Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Sophia Hebron Mwakagenda (5 total)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami nimepata nafasi ya kuuliza swali.

Mheshimiwa Spika, maeneo makubwa sana hasa yaliyomilikiwa na makanisa zaidi ya miaka 50 walishindwa kuyaendeleza na wananchi wakaingia kufanya shughuli za kilimo. Kwa sasa wameanza kuwaondoa wananchi hao ambao wamelima zaidi ya miaka 50. Serikali itasaidia nini wananchi hawa waweze japo basi kugaiwa kidogo waweze kuendeleza shughuli zao za kilimo maana kwa miaka mingi wamekuwa wakiishi mahali hapo? Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Unaweza ukatoa mfano?

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ndiyo. Pia Waziri Mkuu alifika eneo la Ilolo Katika Kata ya Kiwira, Wilaya ya Rungwe, Mkoa wa Mbeya, anafahamu tulilizungumzia suala hilo.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba taasisi zetu za kidini nyingi ziliweza kumudu kuchukua maeneo makubwa sana kwa ajili ya kujenga nyumba zetu za ibada kwenye maeneo hayo. Maeneo kama haya wamemudu kujenga eneo dogo na maeneo makubwa yamebaki, tukiwa tunazungukwa na vijiji na wananchi wanahitaji kutumia na maeneo mengi pia wananchi wameingia humo kutumia.

Mheshimiwa Spika, bado hatuwezi kuacha kufuata Kanuni za Ardhi kwamba unapokuwa na ardhi lazima upate Hati, unapokuwa na Hati unakuwa na kibali cha umiliki wa eneo hilo. Yeyote ambaye atakuja hawezi kupata hati nyingine juu ya hati; na kama atafanya kazi hapo, ajue kwamba eneo hilo siyo lake, bali ni la yule mwenye hati.

Mheshimiwa Spika, mgogoro mkubwa uliokuwepo kwenye maeneo mengi ni huo ukubwa wake na matamanio ya watu kuingia. Mbali ya ziara yangu niliyofanya Mkoani Mbeya Kiwira, lakini nilikuwa Dar es Salaam eneo la Temeke, kuna Kanisa huko la Anglikana, lina eneo kubwa kabisa, Halmashauri wamehangaika kutafuta eneo la kujenga kituo cha mabasi hawana, wameenda.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme, kwanza zipo Taasisi za Kidini zinatambua mahitaji ya ardhi kwa wananchi wanaowazunguka na wanachofanya wanapima uwezo wao hata wa kuendeleza wanawagawia wananchi kidogo kidogo na wanawapa vibali vya muda lakini pia baadaye huko tunaona nia thabiti ya baadhi ya Taasisi za Kidini zikiruhusu wananchi kuwakatia eneo hilo na wapate Hati na kuwaachia kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo yanamilikiwa bado na taasisi hizo. Wizara ya Ardhi inayo Sera yake ya maeneo haya, namna ya kuishi na hawa watu, lakini kutambua kwamba sasa hivi tuna ongezeko kubwa la wananchi na wanahitaji kupata huduma ya maeneo ya kilimo ili waweze kujikimu.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kufuatilia mwenendo wa sheria zetu, tunaendelea kushauri wale waliochukua maeneo makubwa wapunguze maeneo hayo ili tuwaruhusu wananchi; na kwa busara za viongozi wetu wa kidini, wanakubali, wanatoa maeneo yale na kuwaruhusu wananchi waweze kulima na baadaye pia hata kurasimisha wao waweze kuchukua maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ambacho tunakifanya sasa ni Mamlaka zetu za Mitaa kule Halmashauri, wanakaa na hao ambao wamechukua maeneo makubwa na hayatumiki kwa miaka mingi ili wakubali kuyaachia na jamii iweze kunufaika. Kwa hiyo, tunaendelea kuzungumza nao ili waweze kuachia, lakini pale ambapo tutakuja kuimarisha na kusimamia sheria zetu, tutakuja kuimarisha, lakini kwanza kwa haki yake ya msingi aliyonayo, basi lazima kwanza tushauriane naye ili apunguze maeneo na hiyo inatokea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutaendelea kuzungumza na wenye maeneo makubwa, hasa Taasisi za Kidini lakini kwa hao wengine ambao waliita ni wawekezaji, tukakubaliana kwamba katika kipindi fulani atakuwa ameshalima, ameendeleza na hajafanya hivyo kwa miaka mingi, hao sasa Mheshimiwa Rais anatumia nafasi yake kuchukua ardhi hiyo na kuwagawia wananchi ili waweze kutumia kwa manufaa yao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea na busara zote mbili hasa kwenye maeneo ya kidini kuweza kushauriana nao viongozi wa kidini na kwa bahati nzuri wanatuelewa. Kwa hiyo, huo ndiyo utaratibu ambao tunautumia kwa sasa. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, zao la chai lina soko kubwa sana hapa nchini na hata soko la dunia. Nini kauli ya Serikali juu ya wakulima wa chai wanaolima chai lakini chai hiyo inauzwa kwa bei ya chini sana na kuwanufaisha watu wa katikati ambao wao hawawezi kusaidia hawa wakulima wakaweza kukidhi mahitaji yao?

Naomba kauli ya Serikali juu ya bei ya chai hapa nchini Tanzania. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mazao yetu haya chai ikiwemo Serikali inaendelea kuyasimamia kuanzia kilimo mpaka masoko yake na malengo ya Serikali ni kumnufaisha mkulima aweze kupata tija ya kutosha kwa kuuza bei nzuri kwenye masoko yetu.

Nakiri kwamba tunayo changamoto kwenye masoko ya zao la chai, hata tulipokuwa kwenye kikao pale Njombe miezi miwili iliyopita tulizungumza kwa kina juu ya tatizo la soko la zao la chai ambalo kwa sasa minada yake inategemewa sana kufanywa nchini Kenya kwenye Jiji la Nairobi pekee badala ya minada ile kuendeshwa hapa nchini na kuongeza gharama za uendeshaji wa zao hili kuliko kama tungeweza kuanzisha mnada hapa. Makubaliano ambayo tumefanya pamoja na wadau ni kuanzisha soko hapahapa ndani ya nchi ili kuwezesha zao hili kupata bei nzuri kwenye masoko yetu na kuwataka wanunuzi waje nchini wanunue hapa na kwa hiyo itapunguza gharama za uendeshaji wa mkulima mwenyewe na wengi wapo kwenye ushirika na ushirika wenyewe ili bei ile iweze kumsaidia mkulima kuweza kulilima tena zao hili na kulifanya kuwa endelevu.

Mheshimiwa Spika, katika miaka/mitatu iliyopita tumepata changamoto sana, nimetembelea Rungwe kwa Mheshimiwa Mwakagenda, nimetembelea kwenye kiwanda lakini nimezungumza na wakulima pale Rungwe nimeona tatizo kubwa miaka hii miwili/mitatu unaotokana na ugonjwa wa Covid kwamba masoko yetu kule tumeshindwa kuyafikia na kwa namna hiyo hata wanunuzi wamekuwa hawaamini kununua mazao kwa umbali pamoja na kwamba tuna mifumo ya kielekroniki, hata hivyo bei zake zimekuwa za chini sana. Kwa hiyo, tunachofanya hapa, tunaendelea kupunguza hao watu wa kati ambao wanazidi kupunguza faida ya mkulima na kumfanya mkulima moja kwa moja kupitia ushirika wake aingie kwenye mnada ambao tumeupanga kuufanya humuhumu ndani. Hivyo ndiyo njia sahihi ambayo tunadhani inaweza kutusaidia pia kumfanya mkulima apate fedha yake moja kwa moja badala ya watu wa kati ambao wakati mwingine wanafanya thamani ya zao kupungua.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali tunaendelea kuona na kubaini masoko kupitia Balozi zetu kuona ni Balozi ipi nchi hiyo inahitaji chai ili tufanye mauzo ya moja kwa moja na nchi hiyo ili zao letu kwa kweli liweze kupata bei. Kwa hiyo, jitihada za Serikali zinaendelea na niwahakikishie Watanzania kwenye mazao yote chai ikiwemo, tunaendelea kujitahidi kuhakikisha kwamba tunapata masoko ya uhakika ili wakulima wetu wote wapate faida kwenye kilimo wanachokilima na hasa kwa kutafuta mifumo mizuri ya masoko. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana nami kupata nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, magonjwa yasiyoambukiza; cancer, moyo na figo, yamekuwa yakitesa sana wananchi na yana gharama kubwa sana: Je, ni lini Serikali itaamua kuleta ile Bima ya Afya kwa wote ili kupunguza maumivu makubwa ambayo yanawapata kwa sababu gharama ni kubwa sana? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda, Mbunge wa Mkoa wa Mbeya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba magonjwa haya sasa hivi nchini yamekuwa yanasumbua sana; cancer, magonjwa ya moyo, figo, pia hata BP, kisukari, ni miongoni mwa magonjwa ambayo Serikali kwa sasa imeyawekea msisitizo na mkazo kwamba yapewe kipaumbele katika kutoa tiba. Ndiyo maana kwenye sera yetu magonjwa haya kwenye maeneo mengi yanatolewa bure ili mgonjwa anapopata tatizo hili aweze kutibiwa bila gharama zozote.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na mchakato wa kukamilisha kuanza kwa Bima ya Afya kwa Wote. Tayari hatua za awali mpaka Baraza la Mawaziri imeshapitishwa; uko upungufu kidogo unatakiwa uimarishwe. Kwa sababu tunazungumzia Bima ya Afya kwa Wote, tunaendelea kupata uzoefu na ushauri na wadau kwa sababu Serikali ilianza na Bima ya Afya ile ya jamii inaitwa CHF; yako mafanikio na pia upo upungufu. Pia, tukawa na Bima ya Afya ya wafanyakazi NHIF ambayo pia nayo tumepata mafanikio, lakini pia changamoto zipo.

Mheshimiwa Spika, tunapokuja kuzungumzia Bima ya Afya kwa Wote sasa tunaanza kupata ule uzoefu tulioupata kwenye CHF na NHIF ili tuone namna ambavyo tutapanua na kumfikia kila Mtanzania, kila mmoja kwa pembe zote nchini ili tunapoanza Bima ya Afya tusiwe na upungufu mwingi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndiyo hatua ambayo Wizara ya Afya inaendelea nayo kwa kushirikiana wadau, wale ambao wanatoa Bima ya Afya kwenye taasisi mbalimbali nao; hizi taasisi za bima ya kawaida ambapo pia nao wanatoa huduma ya matibabu ili tuweze kuweka utaratibu ambao utatufikisha. Kwa hiyo, Serikali sasa ikishakamilisha magonjwa hay ana wenzetu ambao wanapata tatizo hili tutakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuhudumiwa. Kwa hiyo, nawaomba sana Watanzania mtuvumilie.

Mheshimiwa Spika, pia, Bunge letu tunaliomba lituvumilie, tukamilishe eneo hili ili tutakapokuwa tunaleta Bungeni tayari kwa kuanza, tuanze tukiwa tuna uhakika kwamba hatutakuwa na upungufu mwingi. Hiyo, ndiyo dhamira ya Serikali na tukishakamilisha hilo Muswada ule utaletwa hapa, utapitiwa na Waheshimiwa Wabunge ili tupate sasa mawazo yenu, mchango wenu na maoni yenu ya mwisho halafu tuidhinishe sasa Bima ya Afya kwa Wote iweze kuanza. Huo ndio utaratibu wa Serikali.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Waziri Mkuu swali. Mwaka 1994 aliyekuwa Waziri Mkuu, Ndugu yetu Samuel Malecela, alitoa tamko juu ya mabasi yanayosafiri usiku na kusema yasisafiri usiku. Tamko lile halikuwa na sheria wala sera. Ni nini Serikali sasa inasema kwa kuwa, nchi yetu sasa imekuwa ni nchi ya kati na uchumi unatakiwa uende mbele.

Mheshimiwa Waziri Mkuu unaonaje kwamba, mabasi hayo yaruhusiwe kutembea usiku na mchana ili tuweze kuongeza kipato, na hasa pato la Taifa kwa Watanzania wote kwa kuwa, mabasi yakifanya mchana peke yake tunalala usiku bila kuingiza fedha yoyote? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda, Mbunge wa Mbeya, lakini sio Mbeya Mjini, Mbunge wa Mkoa wa Mbeya, kama ifuatavyo:- (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mara kadhaa tumekuwa tukitoa maelekezo, hasa kwenye eneo la usafiri, kulingana na hali ya usalama iliyoko nchini. Wakati huo agizo hili lilitolewa kwa sababu, mara nyingi mabasi yalikuwa yanatekwa yanaposafiri na tulikuwa tunalazimika pia kuweka jeshi la polisi kila basi linaposafiri ili kuhakikisha kwamba, wasafiri wanasafiri salama.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, sasa usalama umeimarika nchini na Serikali inaendelea kuimarisha zaidi usalama nchini. Umuhimu wa hilo jambo upo, lakini nitawasiliana na vyombo vya ulinzi na usalama kuona kama, je, wamejiridhisha kwa kiasi gani kwa usalama huo, ili tuanze kuruhusu mabasi kufanya kazi wakati wote, ili kuboresha uchumi, lakini kuwafanya abiria kuwa na mipango binafsi ya kibiashara ya kusafiri kutoka eneo moja mpaka eneo lingine katika kuendesha biashara zao kwa uhuru mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika hili lazima pia tutoe wito kwa Watanzania; kudumisha amani na usalama na utulivu nchini ni muhimu sana kwa sababu, malengo yetu ya kuboresha uchumi wa nchi, kama nchi haiko salama hatutayafikia. Wito uliotolewa na Mheshimiwa Mwakagenda unaendelea kusisitiza na kuonesha umuhimu wa Taifa hili kuendelea kuwa salama ili wale wanaoamua kufanya biashara zao wakati wowote wafanye biashara hizo.

Mheshimiwa Spika, pia tumeanza kutoa wito hata kwenye mamlaka ya Serikali za Mitaa kupitia masoko yao makuu kuhakikisha kwamba masoko haya yanafanya kazi masaa 24 ili kuwaruhusu hata wanaokuwa busy mchana kutwa kwenye ofisi zao waweze kufanya hivyo wanapopata muda wa mapumziko ambao pia ni usiku kama ambavyo tunaona kwenye nchi zilizoendelea za wenzetu, watu wanaenda shopping center, biashara zinafanywa masaa 24 na sasa tunataka Tanzania hiyo pia ijitokeze kuanzia kwenye masoko yetu, kwenye usafiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeagiza vyombo vya ulinzi hasa Jeshi la Polisi kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya waendelee kufanya tathmini hiyo kwa haraka ili tupate taarifa hiyo tuweze kutoa vibali hivyo vya kusafiri nyakati hizo ili kazi ziendelee. Ahsante sana.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Waziri Mkuu swali la nyongeza.

Mheshimiwa Waziri mmefanya kazi kubwa sana kupunguza miaka kutoka 11 sasa na kuwa 10 kwa maana ya miaka sita na miaka ile minne ya lazima, lakini kuna mzigo mkubwa sana wa masomo mengi kwa watoto wa shule za awali. Je, kuna utaratibu gani ambao Serikali imeuona wa kupunguza idadi ya masomo lakini quality ikabaki palepale? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mbunge wa Mbeya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Elimu ilipokuwa inatekeleza Sera hii ambayo tunaimalizia muda wake iliaandaa masomo kulingana na uhitaji. Sasa mabadiliko ya sera hii nayo yataangalia mzigo huo na kwa kuwa wadau walishapata nafasi ya kuchangia tunaamini hili nalo walishalisema na Wizara ya Elimu imechukua maoni yote yaliyotolewa na wadau katika kuhakikisha kuwa mzigo huu unapungua na utaratibu ambao upo kwa madarasa ya awali yanayomwandaa mwanafunzi kuingia darasa la kwanza wale masomo yao ni kusoma, kuhesabu na kuandika.

Mheshimiwa Spika, walikuwa wanaandaliwa hivyo kwa kipindi chote cha mwaka mmoja au miwili kulingana na umri wa mtoto. Wanamwandaa kujua kuandika, kusoma na kuhesabu ili aingie darasa la kwanza akiwa anajua kuhesabu, kuandika na kusoma na anapoingia kwa darasa la kwanza, la pili anaanza sasa kuingia masomo ya shule za msingi. Hapa sasa sera na michango ya wadau watakuwa wameshapitia hayo na ushauri upo Wizara ya Elimu, kuona ni masomo yapi yafundishwe kutoka darasa la kwanza mpaka la sita na pia yataangalia uzito na umuhimu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa sasa tunawaandaa kwa ajili ya kuingia kwenye mafunzo ya sekondari, lazima watafanya mapitio tena ya masomo haya ili kutoa idadi ya masomo ambayo yataweza kubebwa na kijana huyu wa umri huu ambaye anasoma mpaka darasa la sita ili kumfanya awe na uelewa mpana na wa haraka zaidi, ahsante. (Makofi)