Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Sophia Hebron Mwakagenda (67 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kabla sijaingia kwenye kuchangia, natamani niwakumbushe Wabunge wenzangu, maana nimeona wakitoa maoni kwamba Wapinzani tulitoka nje siku ya hotuba ya Rais. Waheshimiwa Wabunge, kuna njia nyingi za kufanya advocacy. Tunafahamu fika Bunge letu ni moja ya Mabunge ya Jumuiya ya Madola, tunapotoka nje, ni pale ambapo umeona hoja ulizokuwa nazo aidha zimesikilizwa au hazijasikilizwa. Hivyo kutoka nje siyo dhambi, ni dalili ya kuonesha hisia na mawazo ambayo tunayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza kuzungumzia hotuba ya Mheshimiwa Rais, amezungumza mambo mengi na hata wengine wamesema kwa sababu hatukuwepo hatuwezi kujua ni nini amezungumza. Sisi wote ni wasomi, tunasoma habari za Vasco da Gama lakini hatukuwepo na tunanakili kwenye mambo mbalimbali. Tumesoma mambo ya Hitler tunayatumia na hatukuwepo wakati wa uongozi wake. Vivyo hivyo habari hii itasomwa na sisi, itasomwa na watoto wetu wa sasa na vizazi vijavyo. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Rais ilikuwa ni nzuri kama walivyosema wengine tatizo naloliona ni utekelezaji. Nitajikita katika mambo ya uchumi aliyoyazungumzia hasa katika ukurasa ule wa 19. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika tunapozungumzia kukuza uchumi wa viwanda, nchi ambayo wasomi hatujawaandaa kuwa wabunifu, hatujawaandaa kuwaweka katika hali ya utendaji kazi, inakuwa shida.
Tunapozungumzia uchumi kilimo chetu ambacho watu wengi ni wakulima kwa asilimia kubwa, mazao wanayoyalima hatujajua ni jinsi gani ya kuwapelekea viwanda hivyo kwenye sehemu husika. Binafsi siamini kwa maana najua Magufuli ni mtu mmoja, mfumo wa Magufuli
ndiyo uliooza, atawezaje kufanya kazi peke yake? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, amezungumza mengi na amezungumzia habari ya Katiba. Katiba ndiyo mama na mimi nilifikiri siku 50 za kwanza za Urais wake angeanza na Katiba.
(Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ametamka na namnukuu, anasema, Katiba ni kiporo. Unapozungumzia kiporo kinaweza kikawa kizuri au kikakuharibu, kikawa kimechacha. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Mheshimiwa Rais, Katiba ndiyo msingi wa kila kitu. Hata viwanda hivyo na huu uchumi tunaouzungumzia pasipo Katiba hiyo hatutaweza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, bado naendelea kujikitia kwenye uchumi, amezungumzia wajasiriamali wadogo, amezungumzia wanawake na vijana ambao ni kundi kubwa sana lililosahaulika. Tunawezaje kuwaunganisha wanawake hawa na viwanda endapo elimu yao ni
ndogo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, tunafahamu tuko katika Jumuiya ya Afrika Mashariki. Mheshimiwa Rais sijaona akizungumzia ni jinsi gani tutajua masoko haya ya watu wachache ambao ni wajasiriamali, wakulima wadogo, wataingiaje katika masoko hayo na kuweza kufaidika na Jumuiya hii ya Afrika Mashariki?
Mheshimiwa Naibu Spika, sijaona akizungumzia muunganiko wa vijana kujiajiri katika uzalishaji mali. Tunapokwenda kwenye viwanda, kama ni kilimo wanawezaje kujiunganisha na viwanda hivyo anavyovisema? Ndiyo maana nasema nina wasiwasi na suala hili la viwanda
analolizungumzia Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hii imeelezea mambo mengi yanayofurahisha kwa kuyasikia lakini nafikiria, wakulima na hivyo viwanda anavyovisema, nikizungumzia Jimbo la Rungwe Magharibi kuna wakulima wa chai. Wakulima wale wanapunjwa, wanauzia makampuni binafsi kwa bei ndogo ambayo wawekezaji hao wanafanya kwa manufaa yao na kibaya zaidi wanashirikiana na watu walio katika madaraka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia viwanda, Kiwanda cha Chai cha Katumba ambacho kinaweza kutoa ajira kwa vijana wengi tumekisaidiaje kukipelekea ruzuku na kusaidia wananchi wa mji ule? Kuna viwanda vingi, Mbeya Mjini kulikuwa kuna ZZK, leo hii imekuwa ni
ghala la kuwekea pombe. Tunawezaje kusaidia vijana wetu kupata ajira? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni vyema Mheshimiwa Rais akatazama ni jinsi gani tutafufua viwanda vilivyokuwepo. Watu waliovifilisi pia wapo, tunawezaje tukarudisha vile viwanda vilivyouzwa kwa bei rahisi kwa watu ambao wamefanya maghala? Nadhani Mheshimiwa Rais angeanzia majipu ya aina hiyo kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sheria nyingi kandamizi kwa mfano Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971, watoto wadogo tunasema wanapata mimba lakini sheria haiko sawa. Kabla hatujaenda kwenye mtazamo wa maendeleo lazima tubadilishe sheria kandamizi na nyinginezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sheria za kodi ndogo ndogo zinazowatesa wananchi tunazibadilishaje? Tunawaunganishaje wananchi kuingia katika uchumi na tukasema uchumi wetu umekua, jana tulikuwa tunaambiwa uchumi wetu umekua, kivipi? Tunawianishaje kukua
kwa uchumi mnaozungumza Serikali na maisha ya mwananchi wa kawaida, tunayazungumziaje? Tuondoe siasa tuweze kufanya kazi. Magufuli anayo kazi kwa sababu watendaji wake ni walewale, pombe mpya kwenye chupa ya zamani. Namwonea huruma na sijaelewa atafanyaje kazi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao vijana wengi ambao mpaka leo hii tumeanza kufanya marekebisho mbalimbali, kwa mfano gesi, je, Serikali imepeleka vijana hawa kusoma? Wako wachache tena wa wakubwa mnawapeleka Ulaya, kwa nini msichukue mtaalam kutoka Ulaya
akaja kufundisha watoto kwa wingi hapa Tanzania? Kwa hiyo, kuna vitu vingi tunahitaji kurekebisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia amezungumzia haki, ataangalia makundi ya wazee, walemavu, hakuna haki kama hakuna Katiba bora. Tunaposema haki tunamaanisha ni lazima anayestahili haki apewe. Ndugu zangu wengi wamezungumza mambo ya Zanzibar na
mengine lakini kuna haki ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), hatuoni ni jinsi gani wakisaidiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kusema haya, nafikiri kuna haja ya makusudi kabla hatujaendelea na safari hii tuanze na Katiba, tena siyo pale ilipochakachuliwa, tuanze na Katiba ya Warioba, tuanzie pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, kuhusu umeme; umeme wa REA katika Wilaya ya Rungwe, hasa REA phase lll haijafanyika maeneo mengine na hasa vijijini.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mgodi wa Kiwira. Ni lini mgodi huu utaendeshwa kwa faida ya nchi na Wanambeya? Kumbuka uliajiri vijana wengi hasa wanawake wa Mkoa wa Mbeya.

Mheshimiwa Spika, kuhusu fedha za ACACIA. Ni lini tunalipwa wananchi sawa na ahadi ya Waziri husika? Maana wananchi wa Mbeya tunasubiri gawio.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Namshukuru Mungu kupata nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu sana kwa Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na bajeti, hii nafikiri ni ya nne na sisi Kambi Rasmi ya Upinzani tumetoa mawazo mbadala kuweza kusaidia Taifa letu kusimamia masuala ya uchumi. Tunashukuru kuna wakati mnakubali kuna wakati mnakataa lakini mwisho wa siku Watanzania watajua kwamba sisi tulikuwa tunatoa mawazo kwa ajili ya kusaidia Watanzania wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti zinapotangazwa nchi za Afrika Mashariki kwa siku moja inasomwa na hii imefanywa kimkakati sawasawa na tulivyosaini kama nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Nchi ya Kenya imeweka bajeti yake kiasi cha dola bilioni 30.2. Naizungumzia Kenya kwa sababu mimi binafsi naamini vitu vingi sana tunavyofanya sisi wenzetu wanatuangalia tunafanya nini na sisi pia tunawaangalia wanafanya nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti yetu imefika shilingi trilioni 33, wakati wenzetu bajeti yao ukichukua Burundi, Rwanda, Uganda na nchi zingine za Afrika Mashariki, Kenya peke yake imetuzidi. Kwa nini nazungumzia hilo? Soko lililopo hapa nchini ukienda kwenye spices zote kwenye maduka ya jumla vifaa vya Kenya vimejaa hapa nchini na sisi kama nchi ya Tanzania tunajinasibu ni nchi ya viwanda kwa miaka hii minne hizi bajeti tumezizungumzia ni kitu gani ambacho tumezalisha na kimeuzika katika soko la Afrika Mashariki kama wenzetu walivyofanya? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango na timu yake nzima ni lazima tufanye kazi kimkakati ili kuweza kuinua uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wenzetu wanatangaza bajeti yao sisi Waziri wetu Mheshimiwa Dkt. Mpango anazungumzia tunaelekea kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa ni mtu gani achaguliwe atoke CCM. Wakati huu siyo wa kuzungumzia mambo ya vyama ni wakati wa kuzungumzia mustakabali wa Taifa hili hasa katika mambo ya kiuchumi. Kwa hiyo, naomba Msomi Mwalimu Mheshimiwa Dkt. Mpango simamia sehemu uliyopewa na wananchi lakini na Mungu amekupa hiyo nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna vipaumbele kama Taifa. Katika kipaumbele cha kwanza ambacho nimekisoma kwenye kitabu cha Mheshimiwa Dkt. Mpango amezungumzia suala la kilimo na viwanda. Kinachonishangaza asilimia 40 ya mapato na mgao umeenda kwenye nishati na ujenzi. Kipaumbele ni kilimo ambacho kina asilimia zaidi ya 70 ya Watanzania hawana pembejeo za kutosha, masoko ya mazao yao hata wakilima na network ya hiyo East Africa tunayoizungumzia ya kupeleka bidhaa. Matokeo yake Wakenya wamewekeza maparachichi kule kwetu Rungwe na Mbeya wanalima na wanapeleka kwao wanafanya packing wanaenda kuuza nchi za nje Sweden na sehemu mbalimbali, wakati wananchi wetu sisi wa Tukuyu wanaendelea kuuza kwa bei rahisi maparachichi hayo. Ukisema kipaumbele chako ni kilimo au viwanda tunategemea bajeti uliyoipanga asilimia hiyo 40 ungeiwekeza huko ili iweze kuwa na tija na manufaa kwenye Taiga letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi bado nashangaa Mafisa Ugani katika kilimo ni wachache. Kwa mwaka wa nne sasa ajira hazijakuwepo kupata Maafisa Ugani wa kutosha katika kilimo. Masoko kama nilivyosema, tunatumia SIDO wakati mwingine wanajitahidi kutangaza masoko madogo lakini haya masoko ni watu gani wanapata taarifa kwa wakati? Tumesaini mikataba mbalimbali, biashara kwenda AGOA, watu wetu wanazo hizo taarifa? Tunahitaji kubadilika na hasa kuhakikisha wakulima wanatendewa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbegu zinazouzwa sasa hivi ziko chini ya kiwango. Je, watafiti tulionao, tuna Chuo cha Uyole, SUA, Serikali imepeleka kiasi gani cha pesa ili waweze kufanya utafiti na kuweza kuwasaidia hawa wakulima kutoa mazao bora na yenye tija katika soko la kidunia? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Chuo cha Uyole hakijapata pesa za maendeleo kwa muda mrefu sana na huwezi kuendelea bila kuwekeza kwa watafiti au kwa hawa wataalam. Tuna mazao ya ng’ombe wale wanaozalisha mitamba, vifaa vya kutosha hawana then unafikiria unaweza ukashindana na nchi kama ya Kenya ambayo leo hii wametuacha kwa mbali sana katika bajeti yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeweka tozo nyingi sana ambazo naziita tozo za kuudhi. Mheshimiwa Mbunge mmoja alizungumza jana juu ya peremende na sausage na vitu kama hivyo, wenzetu Wakenya wametazama matumizi ya simu, Wakenya wengi wanatumia simu za mkononi wameona ni bora kutoka asilimia 10 ya tozo waliyokuwa wanadai wamepeleka asilimia 12 angalau zile asilimia 2 pesa inayopatikana iende kwenye afya. Hizo ndiyo akili za kufanya kwa sababu kutokuwa na simu hutakufa, kwa hiyo, kama unataka kuwa na matumizi ya simu basi simu yako utakapotumia pesa inayopatikana ikasaidie afya na hasa mama na mtoto katika Taifa lao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hicho hicho kilimo, pesa za maendeleo bajeti iliyopita shilingi bilioni 98 zilitengwa na Bunge lilipitisha lakini ni kiasi kidogo sana cha shilingi bilioni 41 zilikwenda. Sasa unawezaje kufanya maendeleo wakati pesa ambayo umeitenga haijafika kwa wakati na kuweza kufanya kazi iliyokusudiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipaumbele cha pili tumesema ni ukuaji wa uchumi wa Mtanzania. Mtanzania huyo atakuwaje kiuchumi wakati wanafunzi hawapati kwa wakati mikopo, tunatengeneza vijana wa aina gani na ni uchumi gani tunauzungumzia? Tumesema vijana wanaosoma masomo ya sayansi na hasa wanawake kwa mfano Udaktari wapate mikopo asilimia 100 lakini kuna wasichana wengi wanarudishwa hawajaweza kupata mikopo na hawana uwezo wa kulipa ada, tunatengeneza uchumi wa aina gani? Unapozungumzia kukua kwa uchumi wa mwananchi mmoja mmoja ni pamoja na kujali na kuwa na dialogue na hao watu kuweza kujiendeleza ni jinsi gani tunaweza kupeleka Taifa mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vitambulisho vya Taifa vilizungumziwa wapi, sisi kama Wabunge haikuletwa humu Bungeni, ni uchumi gani ambao mnauzungumzia? Bado tunahitaji Watanzania waweze kuendelea kiuchumi. Baada ya miaka minne ndiyo mnakumbuka kukaa na wafanyabiashara na hii ni kwa sababu hampendi kusikiliza mawazo mbadala mngechukua hatua mapema haya matatizo yasingetukuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Deni la Taifa. Mwaka jana nilichangia hapa nikasema Deni la Taifa limekuwa ni tatizo, naogopa kusema kansa nitaambiwa nifute, limekuwa ni tatizo. Leo hii limefikia shilingi trilioni 51 kutoka shilingi trilioni 49, hii ni hatari. Kibaya zaidi katika kulipa deni hili bado tunaweza kushindwa kulilipa kwa wakati na mwisho wa siku watoto wetu watapata shida sana kulipa haya madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitoa wazo kuhusiana na Deni la Taifa kabla Serikali haijakopa ilete humu ndani sisi kama Wabunge tuone umuhimu wa hilo deni kama linatakiwa kukopwa tupitishe kwa pamoja maana sisi ni wawakilishi wa wananchi. Nadhani ni vyema tukaliangalia hili deni la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakuja kwenye taulo za kike, wewe na mimi kama mama tunaowatetea wasichana na wanawake, leo hii unasema kwamba tumerudisha kodi kwa sababu wafanyabiashara walishindwa, mimi sioni kama Serikali imesimama katika nafasi yake maana ni Serikali ilitakiwa kuwasimamia hawa watu kusambaza au kushusha bei. Leo hii mazao ya Coca-Cola, Pepsi yanauzwa bei moja kwa sababu kuna bei elekezi, Serikali ilishindwa nini kuweka bei elekezi kwenye taulo hizi za kike? Mwisho wa siku kwenda hedhi ni suala la kibaiolojia na mimi sikupanga kwenda hedhi, ni kitu nimezaliwa nimekikuta, kwa hiyo, tusiwahukumu wanawake na mabinti zetu kwa sababu ya hali yao ambayo Mungu amewapa. Naomba Serikali itakaporudi ijaribu kufikiria hili suala na waweze kulibadilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado nina…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono bajeti yetu ya Kambi Rasmi ya Upinzani, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Nafikiri pia ninao wajibu wa kuzungumzia suala la ugonjwa wa corona lakini nitakuwa tofauti kidogo na wenzangu. Ugonjwa huu ni ugonjwa wa Kidunia na ni tatizo linalotuhusu Tanzania na wanaotuzunguka na dunia kwa ujumla. Nataka kumwomba Rais, afikirie tena aweze kufunga mipaka ya nchi kwa sababu; kuna watu wanafika pale Airport wakitokea nje wanarudi nyumbani. Anajua akifika Airport, anaita uber yake anakwenda kwake labda Tabata au Manzese lakini akifika pale anachukuliwa kwenda kwenye isolation, sawa tunakubali siku 14, lakini wanapelekwa kwenye hoteli za gharama na ndiyo maana watu wanatoroka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sijajua ni utaratibu gani unatumika, labda watusaidie na hasa watu wa TAKUKURU, hizi hoteli zimekuwa vetted vipi na kwa nini ziwe hoteli za gharama na Ofisi ya Waziri Mkuu ni ofisi ambayo ina fungu la majanga na maafa kama haya. Mimi nikiwa na corona na nimetoka safari, sijapanga mimi niwe na corona, kwa hiyo ina maana imekuja mimi nikiwa sina pesa. Kwa nini Serikali isifanye maeneo tofauti ya kuwaweka hawa ndugu zetu, wakakaa hizo siku 14 bila gharama hiyo kubwa, dola 150, dola 100, dola 50 hizo ni hela nyingi sana kwa hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafikiri tuna haja kwanza ya kufunga mipaka kwa sababu sisi sio kijiji na wala sisi hatuna TBS ya kuzuia magonjwa yasituingie. Naomba tulifikirie kwa upya na tukae chini kwa upya tujipange na hasa Wizara hii tunayoizungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, naomba niongeze suala la Wizara hii ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu alilizungumza. Ofisi hii imetamka vipaumbele vine, moja ya kipaumbele wanazungumzia uchumi wa viwanda, uchumi wa viwanda bila kilimo huwezi kufanya maendeleo yoyote. Asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima. Usipounganisha viwanda na kilimo huwezi kupata faida yoyote. Tunafahamu kiwanda, mkulima wa korosho amelima korosho, tumeimba wimbo huu muda mrefu sana kwamba hawa watu wanahitaji viwanda vya kubangua korosho hapa nchini, lakini mpaka leo viwanda hivyo bado havijawa tayari. Tuna wakulima wa chai kule Rungwe, kwenye ripoti ya Waziri Mkuu anazungumzia yule mkulima wa parachichi, yule ni mfanyabiashara binafsi. Serikali inahitaji kuwa na kiwanda, inahitaji kuweka miundombinu ya wakulima wa parachichi waweze kuuza kwa bei ambayo yule mfanyabiashara binafsi anapata faida mara nne na sisi tunafikiri tunapata faida kumbe tunamnufaisha mtu mmoja.

Mheshimiwa Spika, kama Taifa tunapozungumzia viwanda ni lazima tukae chini tuoanishe kati ya viwanda na kilimo, kwamba kilimo kinapolimwa na chai inapolimwa tuwe na viwanda vidogo vidogo vya chai. Zao la chai linanyweka nchi nzima. Kama sio Tanzania lakini dunia nzima wananunua chai na wala hatujawahi kusikia soko la chai limeshuka bei. Leo hii Wakenya wananufaika kwa zao la chai, lakini sisi hatuna viwanda, tunapeleka kitu ambacho hakina thamani zaidi. Tungekithaminisha katika nchi yetu tungesaidia wakulima wetu kupata kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia uchumi ambao unaoanisha uchumi wa mtu binafsi na uchumi wa Kitaifa, mimi naweza nikaona kwamba sipati hela kwa sababu thamani ya mali ninazozizalisha hazifanyiki hapa nchini. Kwa hiyo tuna haja kubwa na ya makusudi tuweze kutengeneza uwezo wa watu wetu kuzalisha na kupata wateja na sisi tuna watu wengi, tukijipanga vizuri, soko la ndani bado linatuhitaji. Kwa hiyo, nilitaka nichangie katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nataka niingie kwenye habari ya siasa, nimesikia watu wengi wanazungumza humu ndani. Chama cha upinzani chochote kilichomo humu ndani kipo kihalali na kikatiba. Kubezana sidhani kama ni njia sahihi, tunapozungumzia haki, haki inabeba vitu vingi sana. Leo hii ni nani humu ndani, mimi najua na kama mama kuna akinamama wenzetu ambao ni wabaya waliolea watoto wa kambo, anamshika mtoto wake ili ampige mtoto wa kambo. Ni kweli yule mtoto anafurahi, ndivyo ambavyo wenzetu humu ndani wanafurahi, lakini wasijue wanajenga immune ya kiburi kwa sababu kila siku ukipigwa, kesho tena umepigwa, unajenga kiburi na unajijengea ujasiri, mmetujengea ujasiri unnecessary. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni nani asiyejua kwamba leo hii watu wanafanya mikutano, kundi fulani linafanya lingine halifanyi. Ukiuliza, intelijensia, intelijensia hiyo iko upande mmoja? Intelijensia hiyo iko kwa nani peke yake?

SPIKA: Umesema nani asiyejua? Spika hajui, tutajie kwamba fulani anafanya mkutano na fulani hafanyi.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, unafahamu kwamba kiongozi wako wa chama cha siasa Mwenezi Polepole anazunguka nchi nzima. Mnyika kazunguka Mwanza mmemkamata! Kama ulikuwa huna taarifa nakupa taarifa! Ni watu wangapi wanafanya mikutano? Mheshimiwa Sugu Mkoa wa Mbeya hafanyi mikutano, RPC anakwambia intelijensia inakataa, Tulia juzi tu hata siku nne hazijaisha na corona, yuko na wananchi! Ina maana huoni? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, undugu tuliozaliwa nao, urafiki tuliokuwa nao…

SPIKA: Mheshimiwa Mwakagenda, kawaida ya Maspika wote duniani wao huambiwa!

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, nakwambia.

SPIKA: Ahsante!

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, undugu tuliojengewa humu ndani kuna watu wana ma- boyfriend humu, kuna watu tuna kunywa chai pamoja humu lakini kwa tabia hii… [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

SPIKA: Mheshimiwa Sophia, una hakika? Maana meza yangu haijui hayo…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: … mimi ninaye! (Kicheko)

SPIKA: Meza inakutaka basi utoke wazi maana umeamua kutoka wazi! (Kicheko)

MHE. SOPHIA H. MWAKAENDA: Mheshimiwa Spika, nimetuma barua kwa Mwakagenda, akishaniridhia nitatoa hadharani.

Mheshimiwa Spika, tunahitaji umoja, kujenga umoja ni kazi kuubomoa ni kitu kidogo. Sisi sote tunawakilisha wananchi…

SPIKA: Nafikiri Sophia hapo ulipokwenda ama uendelee ama ufute kwa sababu umelituhumu Bunge na nina hakika magazeti yote yatajaa kwamba watu wana mahawara humu ndani na watu wana wake zao na waume zao na heshima zao. Kwa hiyo ni bora ukajitokeza tu wazi ukaeleza nani na nani ni mahawara humu…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, mimi nimefuta, naomba niendelee.

SPIKA: Basi kama umefuta tunaelewana.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosisitiza umoja ni muhimu, mwisho wa siku sisi ni ndugu tumetumwa na wananchi kuwawakilisha, tufanye kazi kwa pamoja bila kubaguliwa.

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee suala la Tume ya Taifa. Ameizungumza msemaji mmoja kwamba tunakimbilia kusema refa atutetee. Tume ni refa ndiyo wala sio utani! Lazima asimame katikati na sisi tumesema toka mwanzo tungebadilisha kanuni zetu na taratibu zetu,

Mwenyekiti wa Tume akachaguliwa na Bunge hili au na kitu kingine chochote tusingekuwa na malalamiko haya.

Mheshimiwa Spika, kazi ya Tume ni uchaguzi, mwanzo wa mwaka mpaka miaka mitano inapoisha, ndiyo kazi yake. Kazi yao kuhakikisha watu wanajiandikisha kwenye madaftari, watu wanapiga kura na kusimamia uchaguzi na kuhakikisha mtu anayestahili kutangazwa anatangazwa, lakini utakuta siku za kujiandikisha Tume inaweka siku chache. Watu wengi hawajaandikwa, tukienda kule Zanzibar, watu wengi hawana vipande, wameshindwa kujiandikisha kupiga kura ili waje wachague mtu wanayemtaka.

Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Mheshimiwa Sophia pokea taarifa. Waziri wa Nchi.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika,
naomba tu nimpe Taarifa Mheshimiwa Sophia, utaratibu wa Tume katika kufanya jambo lolote ambalo linahusu uchaguzi ni utaratibu shirikishi. Kabla Tume haijaanza kuandikisha wapiga kura, kabla haijaanza kuboresha daftari vyama vyote vya kisiasa vimekuwa vikishirikishwa na vinakuwa na maamuzi ya pamoja. Kwa hiyo naomba tu nimwambie Mheshimiwa Sophia kwamba hicho anachotaka kukisema si kitu cha kweli kwa sababu kila jambo limekuwa ni shirikishi na baada ya ushirikishwaji Tume ndiyo inaanza kufanya kazi na safari hii imefanya vizuri kweli, hata mikoani haikuanza kazi kabla ya kuwashirikisha wadau wote ikiwemo vyama vya siasa na nafikiri hata Sophia alikuwa anashiriki hiyo mikutano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tu nimpe hiyo Taarifa Mheshimiwa Sophia Mwakagenda.

SPIKA: Mheshimiwa Sophia pokea taarifa.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, sijaipokea Taarifa kwa sababu kazi yangu mimi ni kuishauri Serikali na yeye ni Serikali. Namshauri kwamba Tume kazi yake ni kusimamia uchaguzi mwaka wa kwanza mpaka mwaka wa tano. Tunaomba Tume haina kazi yoyote, Tume haishughuliki na corona wala malaria, inashughulika na uchaguzi. Kwa hiyo tunaiomba Tume kuanzia mwaka wa kwanza tunapomaliza uchaguzi iendelee kuwaandikisha watu wapya wanaofikia umri wa miaka 18 ambao walikuwa na miaka 17 wameingia 18 iwaandikishe. Kama kuna watu wamekufa iwatoe kwenye daftari na ukifika wakati tunaenda kwenye uchaguzi sasa, tupate majina mapema. Kwa hiyo, ninachoomba, naishauri Serikali, sio kwamba lazima uchukue Mheshimiwa Jenista, mimi nashauri kama Mbunge ambaye nina wajibu wa kuishauri Serikali na ndiyo kazi iliyoniingiza humu ndani.

Mheshimiwa Spika, Tume ya Taifa bado sio huru na kama wako vizuri, wamejenga reli, wamefanya kazi zote, kwa nini wana wasiwasi na hiki kitu kidogo tu cha kuunda Tume Huru, kwa sababu wakiunda watashinda! Kwa sababu wana madaraja kama wanavyosema! Tunataka tusiwe na doubt yoyote, ndiyo maana tunashauri iundwe Tume Huru ya Uchaguzi na kama uko vizuri, Mbunge unapendwa…

SPIKA: Mheshimiwa Sophia, tangu jana tunauliza, Tume Huru inafananaje? Kila mtu akisimama Tume Huru, Tume Huru…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Hasemi kwa sababu wasiwasi…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika…

SPIKA: Usiwe na haraka, dakika zako tunazitunza.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Ahsante!

SPIKA: Wasiwasi wetu ni kwamba leo huyu mtu atasema refa hatumwamini, mkibadilisha refa atasema linesman, mkibadilisha, Kamisaa, mkibadilisha TFF, sasa Tume Huru hiyo mnayoiongea, wote inafanana? Kila mtu ana picha ya Tume yake au ni nini ili Serikali iweze kukuelewa na kuwaelewa wote wanaoiongelea subject hiyo.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Tume Huru na hasa Mkurugenzi Mkuu na watendaji wengi wanateuliwa na Rais ambaye kikatiba na kikanuni ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi na nchi hii ni nchi ya Vyama Vingi. Kwa hiyo natoa wazo leo, ni vyema wakaomba kazi, tukawafanyia vetting, wakaletwa Bungeni, tukawachagua tukapata mmoja ambaye tunamuamini sisi kama wananchi wa Tanzania na wala sio kuteuliwa na mtu mmoja. Leo hii Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi ndiyo Rais, kesho atakuja mwingine.

MBUNGE FULANI: Taarifa.

SPIKA: Je, ni nchi gani ambayo unadhani ina mfumo ambao Bunge ndiyo linateua Mwenyekiti wa Tume, Sophia.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, tuko kwenye mjadala mpana wa kusaidia Taifa letu, hata kama maongezi yangu unafikiri hayajaenda sambamba lakini wako watu waliopelekwa shule na wanasoma…

MWENYEKITI: Kwa sababu inaelekea unaongelea subject ambayo hujaifanyia utafiti wa kutosha!

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, tuna Kenya…

SPIKA: Kenya bado pamoja na Bunge kushiriki, Rais ndiye anayemteua Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi. Mimi sikatai hoja yenu, mnielewe! Mimi nia yangu ni kwamba yaani mje na vitu ambavyo mmejiandaa, mmejipanga vizuri, mnapofanya presentation mimi siwazuii, unapofanya presentation yako yaani unashuka umejipanga, ndiyo maana tunaanza saa nane ili kuwapa nafasi Waheshimiwa Wabunge kuchambua, kuangalia references na kadhalika na sisi wengine tunajuajua kidogo kinachoendelea kwa hiyo huwezi kutudanganya. Hatusemi kwamba Tume iliyoko ni malaika, lakini ni vizuri kujipanga kidogo na kutoa mifano ambayo, yaani kulisaidia Taifa kweli kwa mtu ambaye umefanya homework yako, unashuka vizuri. Endelea tu Mheshimiwa Sophia.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, kama chama tumeandika barua kwa Msimamizi Mkuu wa Nchi japokuwa tunaona siku zinasogea nafikiri na maelezo unayozungumza wewe ambayo yameenda kisomi na yaliyoandikwa kihalali ili waweze kusaidia Serikali. Tumeshaandika barua.

Mheshimiwa Spika, viongozi wetu wameshiriki na kuongea na Rais wa nchi kutaka kuitwa na kuzungumza na kuwa na maridhiano ili waweze kueleza ni nini wanachokitaka. Naomba niendelee…

SPIKA: As long as hiyo barua hamjaandika kwa Spika wala nakala Spika hamjampa na Waheshimiwa Wabunge hawa hawajui kinachoendelea sidhani kama ni haki kutueleza, maana sisi tunashangaa yaani, hatuelewi ndiyo maana…

Nauliza hiyo kwa nia njema unielewe vizuri.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, Serikali kuna Bunge, kuna Mahakama, tumetuma kwa Serikali, mimi naongea hapa ndani kama Mbunge ndani ya Bunge.

SPIKA: Hebu kaa chini! Huyu ni Mbunge gani asiyejielewa? Kama umeandika vitu kwenye mihimili mingine kwa nini unaongea hapa sasa? Subiri, kama unaongea hapa, tueleze na sisi! Unaongea kuhusu kitu gani ufafanuzi wake ni nini? Barua yenu ina nini na wewe unaongelea nini? Kuna ubaya gani katika ushauri huo? Kuna ubaya gani katika ushauri huo? Sisi barua yako hiyo hatuna, hatuijui! Wewe ndiyo unaijua na huko ulikopeleka. Tunapokutaka sisi tueleze ni kitu gani unaeleza, tunakosea nini hapo?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia Wizara hii katika maeneo matatu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, uundwaji wa vikundi vya kijamii (SACCOS). Mpaka sasa ni vikundi vichache vimeweza kusajiliwa kutokana na uelewa mdogo na kutotembelewa na wahusika kwa maana ya viongozi wa ushirika kutoka katika Halmashauri zetu. Mpango huu wa kusaidia vijiji shilingi milioni 50 binafsi najua kuna vikundi havitakuwa na sifa kutokana na ugumu huo wa usajili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ni habari. Kama nchi tume-sign mikataba mbalimbali ya haki ya kupata na kutoa habari kwa wananchi. Masikitiko yangu ni kwamba, Serikali imezuia vyombo binafsi kuonyesha, kuandika shughuli za Bunge zinazoendelea kwa kigezo cha kuwa na Bunge TV ambayo kimsingi haionyeshi na kama inaonyesha, inaonyesha kwa upendeleo. Isitoshe kuna magazeti yamefungiwa na kama Bunge halijajua makosa yao ili vyombo vingine vijifunze. Nashukuru kuleta Muswada wa Sheria ya Vyombo vya Habari, labda utaleta uhuru katika habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ni mawasiliano. Tumekuwa na vyombo au Makampuni mengi ya Simu, lakini wasiwasi wangu ni gharama zinazotozwa kwa wananchi. Gharama zinaongezeka katika ununuaji wa vocha na wananchi wengi hawana ujuzi wa kitaalam na kupelekea mwananchi wa kawaida kulipia gharama kubwa sana bila uangalizi wa wataalam watetezi wa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ni uingizwaji wa simu feki unaofanywa na wafanyabiashara wachache na kujinufaisha na kuacha wananchi wanaathirika kwa ubovu wa simu hizo na hata hasara ya kuharibika baada ya muda mfupi. Nashauri TBS na wadau wanaolinda haki ya mlaji wafanye kazi yao kwa faida ya mwananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, ni masoko. Tumeingia katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, sijaona kama tumeandaa wananchi wetu hasa wanawake kuingia katika ushindani wa soko. Pia wananchi hawana elimu ya kibiashara hasa ya utalii ukilinganisha na jirani zetu ambao ni washindani wetu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, Rungwe Mashariki ni moja kati ya Miji inayozalisha mazao mengi ya chakula na biashara, lakini tumekuwa na tatizo la masoko na kupelekea mkulima kupata kipato kidogo na kibaya zaidi wanaofaidika ni Madalali ambao wanachukua pesa nyingi kuliko mkulima mwenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, maoni yangu; tujengewe soko kuu la mazao haya ya ndizi na chai, kwenye chai mkulima ananyonywa kwa kupangiwa bei hasa kwa kutokana na kutokuwa na ushindani katika soko.
Mheshimiwa Naibu Spika, mbolea imekuwa tatizo kubwa hasa mawakala wengi sio waaminifu na kupandisha bei mazao kama kahawa yalikwisha kwa kukosa motisha kwa wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, mageti ya mazao ni kikwazo kikubwa kwa wakulima wadogo kwani tozo zimekuwa kubwa sana zisizo na ulinganifu katika utozaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, uvuvi katika Ziwa Nyasa unatoa samaki bora sana ambao ni kivutio cha walaji wengi. Ningependekeza Wilaya ya Kyela itengewa pesa ya kutosha juu ya utunzaji wa mazalia ya samaki na kuongeza uzalishaji na kutoa ajira kwa vijana wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, zao la maziwa; Wilaya ya Rungwe ina mazao ya maziwa kwa wingi, ni lini Wizara itasaidia upatikanaji wa viwanda vidogo vya kusindika mazao haya ili kuongeza thamani ya mazao haya na kupata faida katika mapato ya Halmashauri na ya mmoja mmoja katika jamii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, VETA Wilaya ya Rungwe; Katika Wilaya ya Rungwe hatuna chuo cha ufundi na hii inatupa shida sana katika kuwaendeleza vijana wetu waliomaliza Darasa la Saba na Kidato cha Nne. Rungwe ni Wilaya yenye kutegemea kilimo sana hivyo uanzishwaji wa VETA kutasaidia vijana kujifunza elimu ya usindikaji wa mazao, ufundi wa kutumia mzao kama mahindi, migomba majani yake na kuwezesha kupatikana ajira kwa vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mabweni Wilaya ya Rungwe, upatikanaji wa mimba za utotoni ni shida sana katika Kata za Kyimo Masukuru. Je, Wizara haioni umuhimu wa kuwezesha Halmashauri ziweze kujenga mabweni ili kupunguza vishawishi, ulinzi kwa watoto wa Kata hizi. Nashauri Mkoa mpya wa Songwe upatiwe umuhimu wa kuanzisha vyuo, vikiwemo vya ufundi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Chuo cha Ualimu Mpuguso. Majengo ni chakavu kabisa idadi ya wanafunzi mabwenini siyo nzuri, miundombinu haifai, vitabu havitoshi kabisa. Pia shule ya sekondari Ndembela, Halmashauri imekuwa na deni la shule ya sekondari Ndembela takribani milioni 700 toka kanisa la Adventista Wasabato barua ya maelezo ya msaada ipo katika Wizara ya Elimu mimi nakumbusha Wizara ione umuhimu wa kulipa deni hilo na kuweka commitment kulibeba deni hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, posho na nauli za walimu. Walimu wamekuwa na madeni mengi sana Serikalini, pesa zao za likizo na nauli wafanyapo kazi nje ya kituo wengi wamekopwa na Serikali kwa muda mrefu sana. Kupandishwa madaraja pia imekuwa tatizo kwa walimu kukaa muda mrefu sana na pesa zao za uhamisho pindi wakipata uhamisho posho hizi zilipwe haraka.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipa nafasi na mimi kuchangia Wizara hii, mimi nitazungumizia upande wa ngumi kwa sababu toka asubuni sijaona uwakilishi kwa watu wa ngumi. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ngumi kama ilivyo michezo mingine ni ajira kwa vijana na mara nyingi sana na kwa muda mrefu ngumi iliyoonekana wapiganaji ngumi ni wakorofi, ngumi ni uhuni, ngumi sio kitu sahihi, ninamshukuru kipekee, Mheshimiwa Waziri aliyepita Mheshimiwa Mwakyembe alijitahidi sana na hasa baada ya kumpa ushauri wa karibu aliweza kuitengeneza tasnia ya ngumi angalau kuonekana ipo katika Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye ngumi Waziri aliyemaliza muda wake aliamua kuweka Kamisheni ya Ngumi, siku za nyuma watu wa ngumi wachache wajanja walikuwa wanachukua vijana kwenda kupigana nje ya nchi, unafahamu ili uweze kupanda daraja kwenye ngumi ni lazima umpige adui yako ndipo unapanda cheo. Hivyo wale tunawaita wasimamizi wa ngumi ikiwepo ma-promoter walikuwa wanachukua vijana wetu wanawapeleka nje ya nchi wakijua kabisa hawana uwezo wa kwenda kupambana na wale wanaoenda kuwagombanisha ili tu wale watu wa nje wapande daraja kwa kutumia vijana wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, huo ulikuwa uuaji na ilikuwa ni tabia mbaya sana. Sasa Mheshimiwa Waziri nina kuomba sana ninajua kwamba wako wachache waliobaki wanachukua vijana wetu wanapeleka nje kuwachezisha kwa mchezo ambao hawajakidhi kwa maana ya kilogram. Wapiganaji ngumi huwa tunapimwa uzito wako na uzito wa kwako na mwingine ndio unakuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanakuchukuwawewe wa kilo 59 wanakupambanisha na mtu wa kilo 70 wa Uingereza promoter apate fedha wakati mpambanaji toka Tanzania anakuwa ameumizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tabia hii Dkt. Mwakyembe aliikomesha, lakini bado inaendelea; ninaomba kiongozi wa sasa aisimamie na kuiangalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Kamisheni ya Ngumi, mtu mmoja asubuhi amengumza habari ya majina ya Urais, sijui nani wa Kamisheni, mimi ninafikiri naunga naye mkono kwamba huyo anayejiita Rais wa Ngumi iweze kubadilishwa. Kwa hiyo, ninaomba Wizara muangalie Katiba ya wanangumi ibadilishwe, maana utendaji wao ubabaishaji bado unaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni promoter pia, baada ya kuacha masumbwi, umri umekwenda sasa nimekuwa promoter. Katika u-promoter wangu nimejikita sana kwa mabondia wa kike akina Feliche, akina Asha Ngedere na wengineo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mabondia hawa hawajui mikataba ambayo wanakwenda kuchezeshwa promoter amelipwa shilingi ngapi; huo ndiyo ugomvu wangu mimi na ma-promoter wengine, hata mkisikia natukanwa, jua kwamba mimi ninapambana. Sisi ma-promoter lazima tuoneshe mikataba na wale tunaoingia nao ili mcheza ngumi akienda kupigana ajue anapigania nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mcheza ngumi anatolewa Tanzania anapandishwa basi kwenda Zambia na wala siyo ndege, anafika amechoka, anakwenda kupambana ngumi kwa kutumia nguvu zake, halafu unamlipa shilingi 200,000; hii siyo sawa. Ninaomba Wizara isimamie hilo. Na hasa ma- promoter wa mabondia wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiwa unacheza ngumi ukishapigwa kwa KO mara nyingi thamani yako inashuka, unazeeka hata nyumba hujajenga. Leo hii mimi nimekuwa Mbunge, nashukuru angalau lakini wengine, mabondia wenzangu walioko nje, hawana hata nyumba kwa sababu ya kipato kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninajua Tulia Trust inasaidia sana, ninakuomba sana waone mabondia wa kike, ili uweze kuwasaidia kama ambavyo unasaidia wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba bima za afya kwa mabondia. Serikali tunawaomba kama ikibidi mtulazimishe sisi ma-promoter tuwakatie bima mabondia wetu. Maana wasipokuwa na bima kuna wakati unapigwa ngumi moja unarudi chini ya ulingo hata pesa ya kujitibia huna. Ninaomba ma-promoter sasa waweze kuwalipia mabondia bima ya afya kwa faida ya maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoka kwenye ngumi, sasa nije kwenye TBC. Televisheni hii ni Televisheni ya Taifa na ina manufaa kwa Watanzania wote. Lakini nimekuwa nikimpigia simu Mkurugenzi wa Shirika hili; kuna wakati vyama vya siasa ambavyo ni walipa kodi na wana uhalali na tv hii pamoja na redio, lakini wanapokuwa na shughuli zao ni vigumu sana kukubaliwa kutoka live kama ukiwa chama mbadala na wala siyo chama tawala. Ninaomba sana Mkurugenzi ufikirie, tv hii pamoja redio ni ya Watanzania, tuhudumiwe kwa usawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hivyo tu, usikivu hasa mipakani, bado unasumbua. Ninaomba Serikali iongeze fedha ili tuweze kuongeza usikivu kwa ajili ya Televisheni ya Taifa pamoja na Redio Tanzania ya kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niweze kuzungumzia Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema kila mtu ana haki ya kupata habari, ya kutoa maoni, lakini kwa nyuma kidogo kulikuwa kuna ugumu wa kutoa maoni kwenye mitandao ya kijamii, kwenye redio na vitu kama hivyo. Lakini tunamshukuru Rais, amesema vyombo vyote viwe sawa na akaruhusu baadhi ya vyombo vilivyofungiwa virudishwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, nitumie nafasi hii kuiambia Wizara irudishe magazeti yote, irudishe vyombo vyote kwa…

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Taletale.

T A A R I F A

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa promoter, kabla Mheshimiwa Waziri hajarekebisha hilo neno la rais, ukisema rais sema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mnavyosema Rais tunajua Rais wa Ngumi, ahsante. (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sophia Mwakagenda.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaikubali taarifa hiyo, ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni mmoja, lakini Rais wa Ngumi, Rais wa Yanga, wote hao wafutwe abaki Rais wa Simba. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuendelee, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesema vyombo vyote vilivyofungiwa virudishwe na mimi nakubaliana naye, nami ninasema leo hii kwenye Wizara hii, ninaomba kabisa zile sheria ambazo zililetwa hapa tukazipitisha, kama ikiwekezana Wizara ilete tuweze kurekebisha baadhi ya sheria tulizozipitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano ile sheria ya kukubali haki ya vyombo vya habari irudiwe, marekebisho ya Sheria ya Huduma ya Vyombo vya Habari ile ya 2016, kama inawezekana iletwe tena tuone kama kuna sehemu ya kurekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Makosa ya Mtandao pia nafikiri kuna haja iletwe sasa tuweze kuirekebisha. Dunia ya sasa mtandao uko kiganjani, tukianza kushikana kwa cybercrimes kwamba umeongea kitu hiki facebook, umefanya hivi, haiwi sawa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naomba nizungumzie suala la BAKITA. Tunafahamu kwamba Kiswahili ndiyo lugha yetu ya Taifa, na Marehemu Rais Nyerere, wote hao walizungumzia sana suala la Kiswahili. Leo hii ukienda nchi zingine, kwa mfano Afrika Kusini ilitaka shule zake, vyuo vyake viweze kuwa vinatumia lugha ya Kiswahili. Lakini walioshinda tenda ya kufundisha ni Wakenya ambao wao ni wanafunzi wetu sisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba sana BAKITA ni lazima mchukue nafasi ya kuwasaidia Watanzania fursa mbalimbali ambazo zinajitokeza, muwe wa kwanza na mfanye kwa haraka kuhakikisha hatuachwi nyuma kama waanzilishi wa lugha hii ya Kiswahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninafahamu wengine wamezungumza habari ya sanaa, ni kweli wasanii, wakiwemo waimbaji wa maigizo, wamekuwa wakijitumikisha wenyewe na kufika mahali tunawasifia, ni baada ya wao kutumia jitihada zao binafsi kufika hapo walipofika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii wamezungumza habari ya kuweza kumpigia kura Diamond. Mimi nafahamu yupo mtoto anaitwa Sonia wa Monalisa. Huyu ni binti wa sekondari lakini ameingia kwenye kuchaguliwa na ametaka wananchi tumchague, ni juhudi za bibi yake anatoa Instagram, na mimi ninayemfuatilia ndiyo ninaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Wizara inafanya nini kuwasaidia vijana kama hawa? Wizara inafanya nini kumsaidia Diamond kuweza hata kutangaza kwenye TBC, ndiyo kazi ya Televisheni ya Taifa, wala siyo kusikiliza taarab, ni vyema tukaangalia vitu vya msingi kuliko kuweka vitu ambavyo ni vya kujiburudisha na wala havijengi wala kusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sanaa; mwingine amezungumza, vijana wetu kwa sababu ya kutokuwa na ajira, lakini wakati mwingine wana vipaji, wamekwenda kuingia kwenye sanaa. Leo mtu anaigiza amekaa chini ya mwembe lakini inadondoka nazi, ni kwa sababu ya kutokuwa na elimu. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba tuwasaidie. Ninaomba Wizara itumie fursa ya makusudi kuwasaidia. Wanahitaji kuigiza, lakini hawana elimu, hawana msaada kutoka kwenye Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba, siyo kuunga mkono, lakini ninaomba Serikali ihakikishe inasimamia hayo bila kusahau kuwasimamia ma-boxer wangu. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuongelea Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyotangulia wenzangu kusema Wizara hii inaongozwa na vijana na kwa sababu inaongozwa na vijana wanahaja ya kuacha alama katika Taifa hili, Mheshimiwa Bashungwa watu wengi wamekushauri na mimi pia nakushauri, kuna mambo yanafanyika ndivyo sivyo usipoyasimamia lawama itakupata na utaharibu jina lako na vizazi vinavyofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia TAMISEMI na hasa kwenye eneo la elimu; elimu ndiyo msingi wa maisha na elimu huanzia kwenye msingi, usipotengeneza jamii yako na hasa kwenye elimu ya msingi kwa watoto wadogo kuanzia hapo unakuwa hujajenga Taifa bora. Mimi ninaamini watu waliosoma elimu nzuri toka elimu ya msingi ndiyo wanaofanya vizuri mpaka sasa. Lakini kumekuwa na uzembe wa Serikali kutokusimamia elimu ya msingi kwa watoto wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ripoti ya CAG ya mwaka 2022 inayoishia mwezi wa tatu inasema idadi ya walimu wa shule za msingi wanaohitajika ni zaidi ya walimu 40,000 lakini walimu waliopo ni 23,000 peke yake, huu ni upungufu uko chini ya 41%. Huwezi kuwa na wanafunzi ambao hawana walimu na bahati mbaya sana waathirika wakubwa ni wanafunzi wa vijijini, hao tumewaonea kwa kuwapa walimu na walimu wanaopangiwa kwenda shule za vijijini wanahama kwa visingizio mbalimbali na kuwaacha watoto wale hawana walimu.

Mimi ninasema Mheshimiwa Waziri, CAG alipoenda kufanya ukaguzi kugundua kwamba idadi hiyo ni ndogo na ninafahamu hamjaajiri zaidi ya miaka sita sasa na mnapozungumzia ajira mnaenda kwenye vyombo vya habari kusema tumetoa ajira na kutoa matangazo mengi, lakini uhalisia walimu wanaoajiriwa ni wachache kuliko wanaohitajika. Ninaomba Wizara yako isimamie hili tupate elimu bora.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa dadaangu Mheshimiwa Mwakagenda kwa hoja anayoizungumzia ya ukosefu wa walimu na ni kweli kwamba foundation ya mtoto ni wale watoto wa awali wanatakiwa wapate elimu bora ya awali, mwalimu mmoja anafundisha wanafunzi 180; sasa unaweza ukaona kwa wastani mwalimu mmoja wanafunzi 180 tatizo ni kubwa sana.

Kwa hiyo nampa taarifa kwamba aiweke hiyo kumbukumbu kwa sababu ameongelea mafunzo awali ya mtoto kumjengea msingi kwa hiyo ni tatizo kubwa sana.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sophia taarif.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipokea taarifa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia elimu bila malipo lengo la elimu hii mlipotoa hilo tamko ni kumsaidia mtoto wa kijijini. Elimu bila malipo mtoto asome vizuri bila michango yoyote, lakini Serikali imekuwa haipeleki fedha kwenye hizo shule kwa ajili ya kusaidia, mmetaja fedha kweli kwa umoja wake mnaweza kusema shilingi bilioni 200 tumepeleka lakini ukienda kwenye ile shule mwisho kabisa mwalimu mkuu anapata shilingi 200,000 atafanyia kazi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, elimu hii haiwezi kuleta tija kama Serikali haiwezi kusimamia yale inayoyasema. Ripoti ya CAG hiyo hiyo ya Machi, 2022 inasema zaidi ya Halmashauri 22 zilizofanyiwa utafiti walikuwa wanahitaji vitabu takribani vitabu 6,000,000 lakini shule hizo zimepata vitabu 1,400,000 tu peke yake unaona upungufu wa vitabu kwenye hizo shule kati ya 6,000,000 kwa 1,400,000 ni vitabu vichache sana tunaomba Wizara yako isimamie kwa sababu huwezi kupeleka watoto shuleni bila kuwa na vitabu vya kiada na ziada. Vitabu hivyo ni vya muhimu na vinavyopungua zaidi ni vitabu vya sayansi tunaomba mtusaidie katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ruzuku bila malipo ambayo inapelekwa kwenye hizo shule nimeshasema hapo mwanzo haziendi sawasawa, watoto masikini ndiyo wanakuwa waathirika, lakini udhaifu wa hizo pesa mnazopeleka kuna maeneo yanapata pesa kwa wakati kuna maeneo yanachelewa kupata pesa. Kuna upungufu zaidi ya shilingi bilioni tano katika fedha hizo mnazopeleka za uzuku kwenye hizo shule, shilingi bilioni tano ni fedha nyingi sana zinapokwenda kwa kuchelewa tunaomba mlisimamie suala hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa walimu ni changamoto kubwa sana tumesema hapo mwanzo lakini uwiano wa walimu, amenipa hapa mwongozo uwiano wa walimu sawa sawa na ripoti ya CAG, kuna baadhi ya wamefanya research kuna mahali walimu wanatakiwa 1,300,000 lakini walimu wapo wachache zaidi ya upungufu wa walimu 20,000 mimi ninaomba Mheshimiwa Waziri ulisimamie hilo kwa sababu upungufu na hizo ni Halmashauri chache zilifanyiwa research upungufu wa walimu zaidi ya 20,000 ni wengi sana. Tunaomba muajiri kwasababu wasomi wapo waliosoma tayari na wanazunguka mtaani, hawana kazi, tunaomba tuwaajiri watu wafanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watoto wanaojiandikisha shule ya msingi wanajiandikisha kwa wingi na ninafahamu Serikali imejenga madarasa mengi na watoto wanajiandikisha, lakini katika umaliziaji wa shule elimu ya msingi watoto wengi hawamalizi shule tunaomba mfuate utaratibu kwa Maafisa Elimu wa Wilaya, Mikoa kujua ni sababu gani zinazowafanya watoto wasimalize elimu ya msingi na tumekuwa na watoto mitaani wengi sana ambao sio lugha nzuri kuwaita watoto wa mitaani kwa sababu mtaa hauzai lakini mwisho wa siku watoto wengi wanazurura mitaani, hawana mwelekeo na wakati huo hapa Bungeni tunazungumzia elimu bora, tunazungumzia kujenga madarasa lakini mijini hata hapa Dodoma kuna watoto wanaopita na kuombaomba na sisi kama viongozi tunawaona, hatuchukui hatua yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie ucheleweshwaji wa ruzuku au fedha za maendeleo katika Halmashauri zetu, shilingi bilioni 54.06 bakaa ambayo ilibaki kwa mwaka 2019/2020 zilichelewa kurudi kwenye Halmashauri na katika fedha hizo zilizochelewa karibia bakaa kati ya hizo shilingi bilioni 15 zilikuwa na Mfuko wa Barabara. Sasa usipopeleka na ukapeleka kwa kuchelewa fedha za maendeleo ya Halmashauri tunazungumzia barabara kwa maana ya TARURA ina maana wakulima ambao wao wameshalima na kupata mazao wanategemea wasafirishe kwa barabara hizo hawatasafirisha, na kama barabara ni mbovu wachuuzi wanaokwenda kununua bidhaa hizo mikoani na vijijini lazima bidhaa itakuwa bei juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba fedha za Halmashauri zirudi kwa wakati na wala tusione zikicheleweshwa kwa sababu zisizokuwa za rasmi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ucheleweshwaji huo wa fedha za maendeleo umekuwa ni mtindo wa muda mrefu sana kwa sasa, tunaomba mzisimamie lakini sio tu hivyo wito ambao mimi niwawapa Hazina, Hazina iweze kutoa fedha kwa wakati, kama fedha zimekusanywa na zimekwenda Mfuko Mkuu wa Serikali tunaomba fedha hizo zitolewe kwa wakati ili Mfuko wa Maendeleo wa Wilaya na Halmashauri zetu uweze kupata miradi na kuweza kufanya kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo kuna wakati mnatoa fedha wanafanya kwa hiyo tunaita fast track haraka haraka ili wakimbizane na muda wa bajeti, fedha inakuwa huwezi kupata value for money, lakini pia watu wanafanya kazi kwa haraka haraka kuitisha tender za haraka hapo na uhuni unakuwepo wa kupitisha mambo ambayo sisi kama wasimamizi wa fedha za Serikali hatupendi kuona zinafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwenzangu hapa amezungumzia suala la ukatili wa kijinsia suala hili limekuwa ni kilio kikubwa sana na kwenye ripoti yako umeizungumzia idadi iliyotajwa ya wanawake na watoto wanaonyanyasika ni kubwa sana kama Taifa tusiposimama ina maana hatuna taifa bora hapo baadaye, wanawake mara nyingi tumesikia kwenye vyombo vya habari na tunafahamu sehemu za vijijini hawana vyombo vya habari itakuwaje wanawake wanauwawa wanawake wanapigwa tu kwa sababu hawana usimamizi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante, malizia.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: … hasa Serikali za Mitaa lakini pia na Wizara husika Kamati imetoa ombi juu ya fedha za UVIKO ambazo zilitolewa tunaomba Wizara yako iundwe kamati…

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: …ili fedha hizi zihakikishwe kama kweli zilifanya kazi iliyotakiwa na wala hawaja divert mradi huu. Ahsante
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi kupata nafasi ya kuweza kuchangia bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, mimi nitazungumza zaidi kwenye kilimo; tunafahamu sote kwamba tulikuwa na slogan kama Taifa kwamba kilimo ni uti wa mgongo na bado hata kama hatutaji lakini kiekweli kilimo ndio kinashiikilia maisha ya Watanzania nusu walioko hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anafahamu kilimo cha kizamani cha kutegemea mvua au kutumia akili za babu zetu kimepitwa na wakati. Tunahitaji kuwa na kilimo cha kitafiti. Kule Mbeya tuna Chuo cha Kilimo Uyole takribani zaidi ya miaka minne, mitano walikuwa hawajapata fedha kwa ajili ya utafiti na sisi tunaamini katika utafiti.

Mheshimiwa Waziri ni lazima tuwekeze katika elimu kwa watafiti wetu ambao wamekwishakusoma ili kuweza kuwasaidia wakulima wetu. Ninaomba sana sana Wizara yako Mheshimiwa Waziri imeweze kutoa fedha kwa wakati hasa pale Uyole, lakini tukienda SUA wanahitaji kupata fedha tuweze kufahamu namna gani kama udongo unafaa, tunafahamu tunahitaji mitamba mizuri, tunahitaji wawe na fedha ili wafanye utafiti. Mheshimiwa Waziri kwa hilo naomba uwekeze sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia utafiti huo huo leo hii tuna kilimo cha parachichi. Kilimo hiki kimeleta watu wengi sana toka nje ya nchi sitataja kwa ajili ya mambo ya kidiplomasia, lakini mwisho wa siku kwenye mashamba, vijijini unakutana na wateja ambao wanakuja kununua parachichi hizi. Hicho ni kitu kizuri mimi sikatai, lakini mwisho wa siku tunapata kiasi gani fedha za kigeni kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, je, Serikali inasimamia hawa wateja wanaokuja, wanatenda haki kwa wakulima wetu? Tumekuwa na tabia mbaya sana ambayo inafanywa na wanunuzi hawa, wananunua parachichi halafu wanaziita reject, ni nani anasimamia kama kweli hizi ni reject? Kwa sababu babu anayelima parachichi kijijini kule Rungwe na sehemu zingine za Njombe hawezi kujua kama hii ni reject au siyo reject, kwa sababu yeye kama mnunuzi anaamua kusema hii ni reject na utakuta hiyo reject ni kubwa kuliko yale mazuri na anaondoka na ile reject Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba sana sana usimamizi kwa wakulima wa parachichi, tunaona kuna madalali wengi sana hapo katikati, tunaomba msimamie kama Serikali. Mwisho wa siku kazi hii ni ngumu ambayo mwananchi wa kawaida amejiwekeza, amelima, ametaka kupata faida na familia yake anakuja dalali anakubaliana na mnunuzi kihuni na mwisho wa siku watu wetu hawapati haki anayostahili kuipata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri tunajua kabisa tunasema parachichi ni dhahabu ya kijani, tunafahamu kabisa kule kwetu tulipotoka, tumetoka katika mia zote parachichi kumi kwa shilingi 1,000 sasa hivi angalau zimeongezeka bei, lakini bado Wizara ya Fedha mtusaidie…

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, hawa watu wanapokwenda kuagiza parachichi…

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Sophia ulipaswa uendelee kuongea nilitaka umalize sentensi yako. Maadam umekaa ngoja upokee basi taarifa manake unao huo utayari, Mheshimiwa Cosato David Chumi.

TAARIFA

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi naomba kumpa taarifa mzungumzaji dada yangu Sophia kwamba kwa muktadha huo kama Taifa maana na mimi natoka tunakolima parachichi, tunahitaji kuwa na kitu kama bodi kwa ajili ya ku-regulate zao hili la parachichi. Bodi ya Parachichi kama ambavyo tuna bodi katika mazao mengine.

SPIKA: Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda unapokea taarifa hiyo.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ninaipokea taarifa hii kwa mikono miwili na naiongezea Mheshimiwa Waziri uichukue hiyo taarifa ya Mheshimiwa Chumi na kuifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kabisa kwamba parachichi tumesema ni dhahabu ya kijani, inawapatia wananchi wetu fedha, lakini kumekuwa kuna tozo nyingi ambazo hazina maana kwa mkulima wa kawaida. Ni lazima Halmashauri zetu ijapokuwa sisi Wabunge ni Madiwani katika Halmashauri zetu, lakini tuwe tuna uniform moja ya utozaji wa parachichi. Ukienda Njombe wana aina yao ya utozaji, ukienda Rungwe hivyo hivyo. Tunataka sasa na ndio maana ya bodi sasa ikiwepo inaweza ikatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii wale wanaobeba zile parachichi wenye magari yale ya cooling system yale wanasimamishwa kila mahali, kila wakati na tozo nyingi sana. Mwisho wa siku tutakimbiwa na hawa wanunuzi na wakulima wetu watalima tutarudi kule kwenye mia zote tunakuwa hatujafanya sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba sana, sana, sana, Mheshimiwa Waziri ninarudia tena kusisitiza suala la reject ninaomba Halmashauri uziambie zisimamie watu wetu waweze kupata haki yao, mambo ya reject iwe kweli, mtu wa Serikali pale halmashauri amtetee mkulima ili kujua kama kweli kaonewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakuja kwenye suala la chai, ninafahamu Mheshimiwa Bashe ulikuwa na kikao kwa ajili ya kuhakikisha tunakuwa na mnada kwa ajili ya chai. Pia tunahitaji maabara, lakini mwisho wa siku tunataka tufenye zao la chai liwe la thamani zaidi. Chai inanyweka nchini, chai inanyweka dunia nzima. Leo hii kuna nchi za Ulaya zinanunua sana chai, tunaomba tuwekeze zaidi. Wenzetu wa nchi za jirani, mkulima wa chai ni tajiri lakini leo mkulima wa chai kwenye mikoa yetu hata kumiliki baiskeli ni kazi. (Makofi)

Kwa hiyo, sisi kama Taifa tunahitaji tuwatetee watu wetu, ninafahamu juhudi za Waziri wa Kilimo anazozifanya kwa zao la chai, lakini bado tunahitaji kuongeza nguvu, tunahitaji kuwa na mnada wa chai ambao mlituahidi kama utakuwepo labda unaweza ukatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba sana kuzungumzia suala la kahawa. Tunafahamu kahawa baada ya petroli duniani kunyweka, kahawa inatumia sana sana sana na wananchi dunia nzima. Tunaomba kahawa ruzuku iwepo kwa wakulima wa kahawa pia tozo ndogo ndogo kwa wanao-export kahawa zipungue ili tuwe sawa na wenzetu wa nchi jirani.

Mheshimiwa Spika, tunapoingia katika Jumuiya ya Afrika Mashariki tunahitaji kuwa na uwiano sawa hata tunapoingia kwenye mambo ya ushindani tusiwe tunakabwa sana sisi kwa kodi nyingi kuliko wenzetu ambao wako mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zao la vanilla Mheshimiwa Waziri; vanilla ni zao zuri lakini limeleta utapeli mwingi sana katika Taifa hili. Sote tunafahamu na tunalalamika katika Bunge hili. Wanakuja kuelezea vanilla inauzwa milioni moja, mkulima analima vanilla halafu mwisho wa siku inauzwa shilingi 25,000 hadi 30,000. Naomba msimamie hawa watu wanaojiita wao ndio viongozi wa vanilla wanaposema uongo Serikali iweze kupambana nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie barabara za vijijini. Leo hii TARURA tunaomba muiongezee fedha na hasa maeneo ya milimani yenye Nyanda za Juu Kusini kule kwetu Mbeya kwa mfano, fedha huwezi kumpa sawa na mtu ambaye anatoka sehemu ambayo hakuna milima. Tunafahamu maeneo ya kwetu Mheshimiwa Waziri yana mvua za mwaka mzima almost, barabara zinaharibika zaidi na kwetu ndio tunalima zaidi na tunalisha Taifa hili. Tunaomba TARURA walioko Nyanda za Juu Kusini kote waongezewe fedha kwa kuwa barabara zao zina changamoto nyingi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikitoka kwenye barabara niende kwenye TAZARA. Mheshimiwa Waziri TAZARA ni reli ambayo inasaidia sana hasa watu wa Nyanda za Juu Kusini. Tunafahamu mazao yetu hata bila ya kupitia kwenye malori wakati mwingine tunatumia treni ya TAZARA, lakini bado Sheria ya TAZARA inatubana. Tunafahamu kwamba ilianzishwa kwa Zambia na Tanzania, lakini tunaona wenzetu kidogo kama wanaenda wanasuasua. Tunaomba muweze kuibadilisha TAZARA ikibidi ipate wawekezaji kwa kupitia Tanzania na nchi yetu iweze kunufaika kwa sababu bado sisi tunauhitaji sana na reli hii. Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri tuisimamie kirahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie fedha za mikopo ya wanawake. Ninafahamu nia njema ya Serikali ya kusema sasa fedha zipite kwenye mabenki, lakini bado ninalo swali. Kule kwetu vijijini maana watu wengi wanaamini benki inakuwa na utaratibu wake, ili upate mkopo benki lazima uwe na document, uwe umesoma na ujaziwe na vitu viko kisomi. Je, mtaweka utaratibu wa kibenki kwa maana ya kupitisha fedha lakini mfumo ule ule wa upatikanaji wa vikundi au mtafanyaje?

Mheshimiwa Spika, si tu hivyo bado tunaomba mfanye haraka kwa sababu mnavyochelewa kuleta majibu haraka kuna wanawake walikuwa wameshakopa ambao tayari wana mikopo hiyo pia wanaendeleza biashara kwa sasa wamesimama hawafanyi kitu chochote. Tunaomba Serikali ije kwa haraka sana iweze kuwarudishia hizo fedha kama mfumo wa benki, lakini uwe kwa haraka na waweze kufanya kazi zao.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya nitaunga hoja nikiona kama umekuja na majibu haya ambayo mimi nimeyasema, ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Bodi ya Ithibati, bodi hii imependekezwa kwenye kifungu cha 10(1) cha Muswada. Binafsi naona haijahusisha wadau kwa upana zaidi hasa kwa kuwaingiza wanahabari na wamiliki wa vyombo vya habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri wajumbe hao saba wachaguliwe na wanahabari na Waziri awapitishe. Waziri kapewa majukumu makubwa sana hata kuna maneno “Idhini ya Waziri” yaliyopo kwenye kifungu cha 14(1) na badala yake kuwepo na kifungu cha 14(3) ambacho kinasema “Waziri anaweza kuagiza bodi kurudia mchakato wa kuchagua Mkurugenzi Mkuu ikiwa kutakuwepo na uvunjifu wa kifungu 14(2).
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nashukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia katika Wizara hii. Nafikiri sitakosea kama mwenzangu aliyetangulia.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaendelea, naomba ni-declare interest kwamba mimi nimezaliwa katika quarter za Jeshi...
TAARIFA
MHE. MATTAR ALI SALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.......
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, uko sahihi kwa sababu na wewe umelizungumzia. Naomba ulinde muda wangu. Naendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, nimezaliwa kambini, Jeshi ninalolijua nikikua lilikuwa ni Jeshi makini kwa maana ya kipato. Wazazi wetu walituzaa wengi kwa kuwa walikuwa wakiishi maisha mazuri, walikuwa wakipata mishahara mizuri, tulikuwa tukipata ration kwa wakati na vitu kama hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jioni ya leo naomba nichangie. Tukiangalie bajeti iliyopita, ndugu zetu pesa za maendeleo walichangiwa shilingi bilioni 220 kama sikosei, lakini Serikali iliwapatia shilingi bilioni 40 au 41. Mimi najiuliza, watawezaje kuishi maisha mazuri tuliyoishi zamani kama Bunge imepanga na imepitisha hiyo bajeti na haijaweza kufika kwenye Jeshi waweze kufanya mambo ya maendeleo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia mambo ya maendeleo, tunazungumzia makazi. Wanajeshi wanahitaji nyumba nzuri za kuishi. Ni kweli tumeona, tumetembelea miradi, kuna nyumba zipo zinajengwa, lakini hazitoshelezi. Ninashauri Bunge linapopitisha bajeti tuhakikishe zile pesa zinakwenda kutimiza ahadi tuliyoahidi, wataenda kuifanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Wananchi kama tunavyolisifia, ni Jeshi linalohitaji kuilinda nchi yetu, mipaka ya nchi, lakini pia tunafahamu umuhimu wa chombo hiki; kama tunashindwa kuipatia pesa kwa sababu zozote zile, tutakuwa hatujitendei haki sisi wenyewe Wabunge. Shilingi milioni au shilingi bilioni 41, ni miradi gani wafanye, ni miradi gani waache?
Mheshimiwa Naibu Spika, siasa ni nzuri, lakini tusifanye siasa kwenye vyombo vya ulinzi. Tunapozungumzia bajeti; na hii naizungumzia kwa Wizara nzima, nikimaanisha Polisi, Magereza na Jeshi wenyewe. Pesa wanazopata tuhakikishe zikipitishwa kwenye Bunge hili zikafanye kazi sawasawa na tulivyoahidi. Walipata pesa nusu karibu shilingi bilioni 600 hazikwenda kutenda kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunafika mahali na wengine wameshasema, hawa ni binadamu, wanaweza wakaingia tamaa kwa sababu wakiishi vibaya hawawezi kusimamia uadilifu waliokuwa nao. Ni kweli tutawasifia, lakini ipo siku wanaweza wakaenda pembeni kwa sababu hatujawajali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwamba Mkuu wa Majeshi leo yupo. Wanawake walioko Jeshini, najua kwamba kuwa mwanamke siyo kwamba huwezi kufanya vizuri. Ninaamini wapo wanawake wenye vyeo, ila ninatamani na ninamwomba ikibidi wanawake waongezwe vyeo, siku moja tuwe na CDF mwanamke na sisi Tanzania tuonekane tumesonga mbele. Ninaamini vyeo kuanzia chini vipo, naomba mchakato wa kuwapandisha vyeo ufanyike sawa sawa na utashi wa kazi wanazofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi letu ni mahiri na wenzangu waliotangulia wamezungumzia habari ya Zanzibar. Sitazungumzia huko ila nina swali la kiufahamu; siku za hivi karibuni nimeona viongozi wa kisiasa waliokuwa ni wastaafu wa Jeshi wakiapa kwa kuvaa nguo za Jeshi. Naomba nielezwe ni utaratibu wao au ni kitu gani? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa mdogo, niliona Mheshimiwa Rais Nyerere wakati wa vita vya Idd Amini akiwa amevaa kombati na nguo za mgambo. Nafahamu kuwa Rais Jakaya Kikwete alikuwa Luteni; mpaka anastaafu sijawahi kumwona amevaa nguo za Jeshi. Sijui nimeshau kama ni Kanali au hivyo! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nifahamishwe, inawezekana sifahamu, siku za karibuni Mheshimiwa Rais wetu amevaa nguo za Jeshi. Najua yeye ni Amiri Jeshi Mkuu, hilo nalifahamu, lakini sikuona begani kama amewekwa cheo chochote.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nielekezwe, utaratibu ukoje? Najua ni Amiri Jeshi Mkuu, lakini begani sikuona cheo chochote. Je, ni sahihi?
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoomba, vitu vingi ni ufahamu; ni suala la kuelekezwa. Inawezekana ilitakiwa ifanywe na Marais waliopita, lakini hawakutaka, lakini kama ni utaratibu, tuelekezwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, Wizara hii inahitaji sana pesa na hasa maeneo ya viwanda. Tunafahamu kwamba Awamu ya Tano mnazungumzia viwanda na jeshi hili lina viwanda; naomba bajeti hii, iongeze pesa kwenye maeneo ya viwanda vya Jeshi. Tukiiongezea pesa tunaomba Serikali badala ya kuagiza vitu vya Kichina, tununue kutoka kwenye Jeshi. Wale wanaopata ten percent wakati huu wasiweze kupata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwa kumalizia, Jeshi hili linafanya biashara, mbalimbali na ukusanyaji wa maduhuli. Ushauri wangu, maduhuli haya kwa miaka hii miwili tungeweza kuwaachia iweze kuwasaidia bajeti zao. Nasema hivyo, ninajua Serikali haina hela. Bajeti imeshuka, tukiwaachia maduhuli kwa miaka hii miwili waweze kufanya kazi zao vizuri, itatusaidia kama Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapopitisha bajeti, hatupitishi kishabiki, tunapitisha tukimaanisha ujenzi wa Taifa. Namwomba Mheshimiwa Waziri, maduhuli ya Jeshi yabaki kwenye Jeshi kwa miaka miwili. Ikipita miaka miwili, tutaendelea na utaratibu mwingine, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, ninaipinga bajeti hii kwa asilimia mia moja kabla sijachangia. (Makofi)
Kwanza kabisa naomba nitoe masikitiko yangu kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya mchana huu kusitisha wanakijiiji wa Mpuguso wasiendelee kujenga zahanati ya nguvu ya wananchi. Ikumbukwe kwamba Waziri wa Afya alipita na akaona wanakijiji akawaeleza waendelee kujenga kwa sababu aligundua kuna ufisadi unaofanywa na watu wa Halmashauri ya Rungwe Magharibi.
Ndugu zangu, binafsi ninaona Taifa kama linayumba, linayumba kwa sababu ya kutetea vyama na Wabunge tuko mahali hapa kutetea haki za wananchi, vyama tumeviacha milango lakini masikitiko yangu ni kwamba imekuwa hali ya kawaida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika Waziri Mkuu hayupo, nilitaka kumwambia wanaopiga makofi wengi wapo zaidi ya miaka kumi katika jengo hili, walipitisha bajeti zilizopipita, wengine waliandika risala za Rais aliyepita, leo hii wanajinasibu kusema uongozi uliopita ulikuwa haufai, kana kwamba uongozi uliopo sasa umetoka mbinguni na wao ni moja ya viongozi waliokuwepo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uzalendo unaumbwa kwenye nafsi na uoga ni dhambi. Ukiwa kiongozi mwoga huitendei haki nafsi yako binafsi, huitendei haki kizazi kinachokuja na ni aibu kwa Taifa unaloliongoza. Leo hii tunazungumzia maendeleo, ni maendeleo gani yanaweza kufanyika pasipo utawala bora? Kama Mkuu wa Mkoa, kwa matakwa yake binafsi na utashi wa chama chake anaweza kuzuia zahanati inayotaka kusaidia wanawake wanaojifungua kwa shida, wapate sehemu murua ya kujifungulia anazuia kwa mantiki ipi na kasi ipi mnayoizungumzia ya hapa kazi tu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa siku tutapita, walikuwepo watu walipita, na wengine mko humu mlikuwa Mawaziri leo mko pembeni. Nchi hii ni yetu sote, nchi hii tulizaliwa hapa, tuko hapa; mnazungumzia habari ya tv, mimi ni mtoto wa uswahilini, leo niko kwenye Bunge hili sikuwepo Bunge lililopita lakini nilichaguliwa, jambo la msingi tumesaini mikataba ya nchi mbalimbali ya haki za binadamu ndiyo maana tunadai tv, siyo kuonesha sura zetu, kama ni sura zinafaamika kwa waliotuoa, wanaotupenda, ndugu zetu, sura zetu wanatufahamu. Tunachosema ni haki ya msingi tunapozungumzia utawala bora ni haki ya msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la elimu. Ndugu zangu TAMISEMI, walimu wanadai madeni, tumewakopa walimu, walimu hawajalipwa mishahara, wengine fedha za likizo kwa muda mrefu, tumewakopa. Bajeti iliyo mbele yetu haioneshi kama inaenda kulipa madeni, na walimu wako wengi katika Taifa hili. Unataka kutengeneza Taifa la viwanda, usipomtengeneza mwalimu ni nani ataingia katika hivyo viwanda? Walimu hawana nyumba, mmeeleza idadi ya nyumba mlizojenga lakini nyumba ni peanut, ni nyumba chache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuwe serious, tusifanye sanaa kwenye maisha ya watu, tusifanye sayansi kwenye maisha ya watu. Mimi nakubaliana kwamba kama nchi iliharibika, nilitegemea Serikali ya Awamu ya Tano itangaze janga la Taifa kwamba tumeingia hatuna fedha, mafisadi wamekula fedha, tunaanza sifuri tujifunge mkanda, ningewaelewa, kuliko kujidanganya kwamba tuna fedha wakati tuna madeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wametukatia fedha za msaada ndugu zangu, Mwalimu Nyerere aliwaaminisha wananchi wakati wa vita vya Kagera, wananchi walimwelewa, wengine walitoa mali zao kusaidia Taifa. Namshauri Mheshimiwa Rais Magufuli kutangaza hali ya hatari, tangaza hali ya hatari kwamba Taifa halina fedha. Tuweke vipaumbele vichache, vitakavyotekelezeka, wananchi watatuheshimu, kuliko kusema tuna fedha nyingi TRA inakusanya fedha nyingi wakati mnajua ni madeni. Mtu unayemdai akikulipa mwisho wa siku analipa nini siyo ameshalipa? Tutabaki kwenye sifuri.
Mheshimiwa Mwenyeketi, vyanzo vya mapato kwenye Halmashauri kuna mianya mingi sana ya upotezaji wa fedha, ninashauri tujikite kukusanya fedha vizuri, tuache siasa. Halmashauri zilizoshinda kwa vyama pinzani zipewe msukumo wa kuendeleza kazi na zilizoshinda kwa CCM zifanye kazi kwa faida ya wananchi. Ubabaishaji wa vitisho vya Wakuu wa Wilaya wanaoingia kwenye Halmashauri za Madiwani sijui kwa vifungu ngani na kuwatisha baadhi ya Madiwani sidhani kama ni muafaka kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua mmetukejeli sana na mkasema hatutaki kuchangia tulinyamaza, tunapochangia mnatuwekea miongozo, mwisho wa siku Taifa ni letu sote, Taifa ni la Watanzania, ninyi siyo malaika na wala tusimfanye Rais kama hirizi, kila kitu Rais, Rais ni Taasisi inawategemea ninyi mkiwa waaminifu mtamsaidia Rais kutimiza ndoto zake. Leo hii Rais hata kama anafanya vizuri yuko peke yake, ninyi wengine...; potea mbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi wengine ni kama wapambe ninaomba mbadilike. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu Tanzania mpya tutaitengeneza sisi, Tanzania mpya haitatusaidia tukipeana vijembea au kwa mabavu, ninaomba tujitafakari kama Taifa, tutetee Taifa letu wala siyo matumbo yetu, tutetee wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya siungi hoja kwa asilimia mia moja na naendelea kusema siku moja ukweli huu utajulikana. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na matatizo makubwa nchini juu ya ulipaji wa fidia kwa wananchi pale Serikali inapotoa/kuchukua ardhi kwa maendeleo na kuwa kero kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi ya jeshi yamekuwa na migogoro kwa jeshi kutokuwa na hati za ardhi zao na wao kusema wamevamiwa na wananchi. Nashauri majeshi yote Polisi, Magereza na JWTZ wapewe hati miliki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Nyumba (NHC); nashauri mikataba yote ya nyumba iliyoingiwa na NHC na wawekezaji wengine ikaguliwe upya. Wasiwasi wangu imekabidhiwa kwa mkataba wa muda mrefu na kwa gharama kubwa mpaka Serikali itakapopata faida itakuwa ni miaka mingi.
Kuhusu maeneo ya wazi, Wizara ikague na kuwanyang‟anya wale wote waliopewa maeneo ya wazi na kuyarudisha kwa wananchi. Maeneo mengi ya michezo na kupumzika yametekwa na waporaji wachache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upimaji wa ardhi. Halmashauri nyingi zimekuwa zinatoa tender kwa wadau kuweza kupima viwanja, nadhani ni kuiibia Serikali mapato yake na kuongeza gharama kwa wananchi. Ninachoomba Wizara ipewe pesa ya kutosha kuweza kusaidia huduma hii kuendelea na kufanya kazi zake kwa urahisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ofisi za kanda; kumekuwa na migogoro mingi ya ardhi katika mikoa hasa ya wakulima na wafugaji na maeneo ya vijijini mfano Kijiji cha Mpuguso, Wilaya ya Rungwe, wamenyang‟anywa ardhi yao ya kijiji na kujenga zahanati huku wakiwa na hukumu ya halali lakini bado wako kwenye usumbufu. Hivyo, naomba wahusika hasa ofisi ya kanda ifanye kazi yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iwe makini kwa hati zinazotolewa kwa wawekezaji ambao wengi wanaingia na gear ya kuoa Watanzania ili waweze kupata ardhi. Kwa kushirikiana na Uhamiaji Wizara inaweza kuwabaini wawekezaji hao.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, vivutio Wilaya ya Rungwe; Wilaya ya Rungwe ina vivutio vingi sana ikiwepo Ziwa Ngozi, Mlima Rungwe, Daraja la Mungu, Kijungu na vivutio vingine vingi sana. Tatizo Wizara haijasaidia kutengeneza miundombinu ya kuwezesha watu kuja kutembelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ziwa Ngozi limeachwa chafu na kutoa tozo ndogo ambayo haiwezi kuleta maendeleo yoyote. Halmashauri zetu hazina pesa ya kuwezesha kutangaza vivutio hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu misitu; Wilaya ya Rungwe tuna misitu ya kienyeji ambayo kiuchumi haina faida kwa wananchi wa kawaida. Vyura wa Kihansi tunaomba vyura hawa warudi Tanzania na nchi ya Marekani ilipe gharama kwa kukaa nao kwa muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wachina na meno ya tembo; kumekuwa na wimbi la Wachina hapa nchini wakikutwa na nyara za Serikali hasa meno ya tembo, swali langu Serikali inachuakua hatua gani ya kisheria kwa wananchi hawa, je, toka wameanza wamekamatwa wangapi na wamefungwa miaka mingapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upandaji miti na nyuki ninaomba Wizara chini ya kitengo cha upandaji miti kunisaidia miche ya kupanda kwa makundi ya vijana, katika Wilaya ya Rungwe na Mkoa wote wa Mbeya. Pia mgogoro wa wafugaji Wilayani Mbarali, je, Serikali itaumaliza lini?
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo kimepungua hadi 2.7% wakati malengo yalikuwa kikue kwa 6%. Hii inaleta wasiwasi hasa kwa wanawake ambao ni wengi katika sekta hii. Sekta hii ni muhimu sana kwani wanawake ni wadau wakubwa sana na mpango huu umejikita kwenye viwanda, hivyo kilimo kiwekewe kipaumbele cha 100% ili kiakisi na viwanda na wakati huo kitaleta tija kwa viwanda vyetu. Maskini wengi wako vijijini ambapo wengi ni wanawake.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumuko wa bei; mwaka 2011 mfumuko wa bei ulikua kwa 19.8%, mwaka 2015 ulishuka kufikia 5.6%, hii ilikuwa sawa lakini kwa sasa imefikia tena 19% na kuleta mkanganyiko kwa jamii maskini. Mfumuko wa bei una madhara mengi kwa jamii hasa wanawake. Nashauri mfumuko ubaki kwenye tarakimu moja kwa kadri inavyowezekana na ikibidi wanawake wakingwe kwa gharama yoyote. Iwepo mipango mahsusi ya kupeleka maendeleo kwa wanawake kwenye vikundi vyao mbalimbali ili kuweza kuzalisha mali kwa maendeleo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nguvu kazi ya utaalam; kuna upungufu mkubwa wa takwimu zilizochambuliwa kwa mtazamo wa kijinsia. Maeneo ya miradi mikubwa ya kiuchumi kama miradi ya Mchuchuma na Liganga ingepewa watu mahsusi na kuzingatia jinsia kutoa wataalam.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Ofisi ya Makamu wa Rais ipatiwe bajeti yake yote ili iweze kutimiza kazi zake kiukamilifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Uchaguzi Zanzibar, Serikali ya Muungano haitaki kuiacha Zanzibar huru ifanye kazi zake kwa matakwa yake bali Tanganyika inaingilia chaguzi na hata maamuzi ya Wazanzibari hapa na pale. Inaendelea kuikandamiza CUF katika utendaji kazi za kisiasa na kero za Zanzibar bado mpaka sasa zinasuasua na sina hakika kama ziko tisa .
Mheshimiwa Mwenyekiti, usalama wa raia toka uchaguzi wa mwaka 2015 Zanzibar haiku shwari kwani ule umoja wa Wazanzibar kwa sasa haupo baada ya kuwa na makundi mawili mahasimu wa kisiasa yaani CCM na CUF.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wengi na wananchi waliumizwa katika marudio ya upande mmoja wa CCM na kuweka ari ya sintofahamu kwa raia baada ya Jeshi la Polisi na JKU kutanda mitaani na kutishia raia. Huu si utamaduni wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katiba mpya; ni wazi tumepoteza pesa nyingi sana kwa kuanzisha mchakato huu kwani matakwa ya wananchi hasa ilipotokea kuachwa kwa rasimu ya katiba ya Mheshimiwa Warioba ambayo CCM iliacha na kutengeneza rasimu isiyokuwa na matakwa ya wananchi. Naomba tuanzie pale wananchi walipotaka kwenye katiba ya Warioba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi za kusingiziwa; kumekuwa na mashtaka ya kubambikiwa kesi katika Serikali ya Muungano hasa kwa wafuasi wa CUF. Tunaomba Wizara hii ichukue nafasi yake ya upatanishi na kusimamia haki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ujenzi wa Madaraja; nashauri Serikali na Wizara hii kuweka kipaumbele cha ujenzi wa madaraja yaliyo katika mipaka ya nchi hasa Malawi kwani hakuna madaraja yatakayoweza kusaidia tukipata dharura kama nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usumbufu kwa magari katika mpaka. Kumekuwa na usumbufu wa foleni ndefu katika mipaka hasa magari makubwa ya usafirishaji ya transit.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa vya Uokoaji. Kumekuwa na uhaba wa vifaa vya uokoaji majini hasa katika boti katika ziwa Tanganyika. Tunaomba Wizara ihakikishe inaweka vifaa hivyo kwani waathirika wakubwa ni wanawake na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha ni kidogo katika Halmashauri ya Rungwe. Katika Wilaya ya Rungwe hakuna fedha za ujenzi/ukarabati wa barabara za ndani wakati Halmashauri hii ni muhimu kwa mazao ya chakula yanayozalishwa hapo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, TBC. Televisheni ya Taifa haifanyi matangazo kwa usawa hasa inapochukua matangazo ya kisiasa kwa uwiano sawa na vyama vingine. Pia TBC ijikite kutoa elimu ya uraia na mendeleo zaidi katika vipindi vyake badala ya kuweka vipindi vya muziki kwa muda mrefu zaidi.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee viwanja vya michezo mikoani. Katika Mkoa wetu wa Mbeya hatuna viwanja vya kutosha vya michezo vinavyoweza kusaidia watoto wetu kujifunza michezo na kukuza vipaji kama mjuavyo Mbeya na viunga vyake bado vinatoa wachezaji bora wa michezo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, niongelee viwanja vya wazi. Viwanja vingi vimetaifishwa na watu wachache bila kuchukuliwa hatua za kisheria na kurudisha viwanja hivyo kwa wahusika ikiwemo Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, vazi la Taifa. Ni lini vazi la Taifa litakuwa tayari katika utekelezaji wa utumiaji huo. Kama Taifa tunahitaji utambulisho wa vazi letu.

Mheshimiwa Spika, sasa niongelee kuhusu timu ya mpira wa miguu. Tumekuwa jamii na Taifa la kushindwa kila wakati kwa Wizara kutowekeza zaidi katika timu hii, lakini Wizara kutosimamia miundombinu/aina ya namna ya kupata wachezaji bora toka sehemu mbalimbali ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, mwisho niongelee suala la ufungiaji wa wanamuziki. Siku za hivi karibuni Serikali imekuwa inawafungia waimbaji wa nyimbo za bongo fleva kwa kile kinachodhaniwa hakiwafurahishi watawala. Hii inaondoa ubunifu na hali ya wasanii kuimba hisia zao kwa usahihi. Serikali itumie ofizi zake kama BASATA kuwasimamia wasanii hawa kufuata kanuni na haki za wasanii bila kubagua na kupendelea kwa kutumia hisia za kisiasa tu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kuhusu utalii katika Jimbo la Rungwe. Tuna utalii katika Wilaya ya Rungwe ambao Serikali haijaweka mkazo katika uendeshaji wake na kuisaidia Serikali kuongeza mapato. Vivutio hivyo ni Daraja la Mungu na Lake Ngozi, vivutio hivi havina miundombinu ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kutangaza utalii nje ya nchi. Serikali iongeze pesa katika Wizara hii ili tuweze kujitangaza na kupata wageni wengi hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hifadhi ya Kitulo haitatunzwa na Serikali kwa kupeleka pesa kidogo hivyo nashauri pesa zitengwe za kutosha kuweza kuitunza hifadhi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, misitu yetu, tunaomba Serikali itoe vibali kwa wazawa ili kuweza kuuza nje ya nchi miti na mazao yake na hivyo kuweza kuongeza kipato cha mwananchi mmoja mmoja na hatimaye wa Taifa.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kabla sijachangia ninaunga mkono hoja ya Kambi ya Upinzani, nafikiri ripoti yetu iko sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapoendelea nataka nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, nafahamu amefanya kazi kwenye NGO’S, hiyo peke yake inamsaidia kum-shape na kumfanya akafanya kazi vizuri ikaweza kumsaidia kidogo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumzia na Wabunge wenzangu wengi wamezungumzia matatizo ya mimba za utotoni. Tumepiga kelele tukijua kwamba mimba za utotoni janga la Taifa hili, kila Bunge linalopita tunazungumzia habari hii. Ndugu yetu amepeleka kesi Mahakamani ameshinda lakini Serikali imekata rufaa. Mheshimiwa Ummy Mwalimu, kuweka alama katika Wizara yako tusikubali sisi kama wanawake, kwa namna yoyote, iwe ya dini, iwe ya mila, itakayopelekea watoto wakapata shida katika umri mdogo na kupewa mimba. Ninaomba tupambane na tukubaliane kabisa, hatutakubali watoto wetu wakiolewa, sasa hivi inafika mpaka miaka tisa watoto wameingizwa kwenye ndoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakupongeza pia kwa kuanzisha kanzidata katika Wizara yako kwa upande wa mambo ya kijinsia, nafikiri hilo ni suala la kukupongeza. Bado kuna shida, tunapofanya udahili, kwenye hotuba yako ukurasa wa 81 umeelezea jinsi tutakavyofanya udahili wa wanafunzi katika Vyuo vya Udaktari, watoto wa kike ambao tumewashawishi wasome sayansi wanapokuwa vyuoni hawana pesa za kulipia mikopo japokuwa wanafanya vizuri darasani na tunajua kabisa tuna uhitaji mkubwa sana wa madaktari katika Taifa letu. Ukienda Chuo cha Kairuki kuna wasichana wameacha shule mwaka wa pili kwa kushindwa kulipa ada za masomo yao. Tunawezaje kusaidia wanawake hawa na Wizara hii kama ni Wizara husika ikawasaidia wasichana wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najaribu kukumbusha, Wizara ikahamasisha uanzishwaji wa nyumba salama (safe home), hizi nyumba salama zitasaidia wasichana wadogo, wanawake ambao wamefanyiwa ukatili wa kijinsia wakati wakishughulikiwa masuala yao, wapate sehemu sahihi ya kusubiri, wakati mambo yao yakishughulikiwa. Ninafikiri Wizara hii ni wakati muafaka sasa wa kuhamasisha. Kuna wadau binafsi wamejitokeza na wameanza, nachukua nafasi hii kumpongeza huyu Dada Janeth Mawinza wa Mwananyamala, yeye amejaribu kuwa na safe home kwa ajili ya wale akina mama wanaopigwa au wale wasichana ambao wanafanyiwa ukatili na baadaye wakaenda wakawahifadhi. Wizara lazima mtambue watu kama hawa, lakini ni wajibu wenu wa kuanzisha vituo kama hivi.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la wanawake na uchumi. Hii Wizara inazungumza mambo ya wanawake na kuwatetea. Leo hii tunazungumzia Benki ya Wanawake binafsi nimefanya kazi na Benki ya Wanawake. Mwaka jana Mheshimiwa Ummy ulimwambia Meneja atoe maelezo jinsi gani anafanya kazi, sasa sikujua kama ni siasa au alikupa maelezo na wananchi haujatupa mrejesho ulifikia wapi. Benki hii ina-charge kama benki za kawaida. Inatoa riba kubwa kama benki za kawaida, jina lake ni tofauti na matumizi ya wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu Mbeya benki hii ina mawakala, lakini Mikoa kama Mbeya, Mwanza, Mikoa mikubwa lazima ingekuwa na matawi makubwa na kuweza kusaidia wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wengi wamezungumza vijijini ambako kuna asilimia kubwa ya wanawake benki hii haijafika, tutaendelea kufanya siasa au tutaendelea kusaidia wanawake.

Ninaomba Mheshimiwa Ummy pamoja na Mkurugenzi wa Benki ya Wanawake fanyeni hima…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana wanafunzi wanaopata mimba za utotoni warudishwe shuleni kwani wengi wao wanapata mimba wakiwa na umri mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mikopo elimu ya juu; mikopo ya elimu ya juu inatolewa kwa wanafunzi wachache na wengi wenye uwezo kuachwa hasa watoto wa kike wanaochukua kozi ya Udaktari na Engineering.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya ufundi vyuo ni vichache hasa Mkoa wa Mbeya, kwani nchi yetu inajinasibu kuingia katika uchumi wa viwanda na tuna wanafunzi wengi wanaishia elimu ya msingi na elimu hii ingesaidia kuwapa elimu vijana wetu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema Serikali ikatoa fedha kwa wakati za maendeleo kwa Jeshi letu ili liweze kutekeleza majukumu yake ya kila siku, kwani kwa kuchelewesha, tunarudisha nyuma maendeleo ya Jeshi letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshangaa kuona maduka yenye gharama nafuu yaliyokuwa yanasaidia familia hizi yamefungwa. Naomba Serikali itoe majibu, ni kwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wetu walioajiriwa kwenye Shirika la SUMA JKT hasa kwenye ulinzi wa makampuni, wanalipwa kiasi kidogo cha mshahara kwani hii linaweza kuleta ushawishi mbaya wa vijana wetu na kuweza kuleta madhara kwa makampuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Mzinga ni muhimu kwa Taifa na Jeshi lenyewe, ila hakipati fungu la kutosha kutekeleza majukumu yake na kwa kuwa Serikali hii imetangaza mwaka wa viwanda, inabidi iwekeze sana kwenye kiwanda hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba Serikali ifuatilie hati miliki za makambi yote ya Jeshi ili kuondoa sintofahamu na wananchi wanaovamia makambi hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya 2000 Jeshi lilianzisha shule za sekondari nyingi na zilisaidia sana kutoa elimu bora kwa vijana wengi na hata michezo ilifanyika na kutoa wachezaji bora. Hivyo, Serikali iendeleze uwekezaji huu kwani ni muhimu kwa Taifa hili.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi nichukue nafasi hii kuweza kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi ninayo maswali kwa Waziri atakapokuja hapa kuhitimisha. Tunataka tujue, Jeshi lina madeni makubwa sana linayodaiwa na watu waliohudumia Jeshi. Sasa sifahamu ni lini Serikali itaweka pesa tunazozipitisha hapa Bungeni na kuhakikisha fedha hizo zinakwenda kwenye Wizara hii kuweza kutimiza majukumu yao? Leo hii mnajinasibu kwamba mnahitaji Jeshi lisiaibike, lakini wakati huo huo shilingi bilioni 200 lakini mnatoa chini ya asilimia 14. Sielewi mnaongea nini na mnafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, tunafahamu Kiwanda cha Nyumbu ni sehemu ambayo Tanzania yetu ingweza kujivunia, wanatengeneza magari, lakini ukifika pale utashangaa sana mashine ni toka Nyerere yupo, alipokuwa akitegemea mkonge na sasa tuna dhahabu. Mnasema Tanzania ya viwanda, kwa nini tusiwekeze kwenye jeshi pale upande wa nyumbu tukaona hiyo dhamira ya viwanda ikitekelezwa kwa kutumia jeshi lile? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda pale vifaa havifanyi kazi, mashine ni mbovu, lakini pesa bado ni ndogo. Ndugu zangu mimi ninaomba tuache siasa katika mambo ambayo ni ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huohuo wanajeshi hawa, amezungumza aliyepita, unawezaje kuhamisha wanajeshi ukawaleta, ni kweli wao wanatii, wakati wa kuhama unaambiwa uondoke asubuhi unaondoka, lakini ni lazima tufikirie hawa watu wana familia zao! Mheshimiwa Waziri utakapokuja kutujibu, utuambie ni lini wanalipwa, kwa sababu si kweli kwamba tunasubiri bajeti hii; kama pesa ni za bajeti iliyopita lazima utuambie wanalipwa lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapinga UKIMWI kama Taifa, leo mwanaume mwanajeshi yuko Dodoma, familia yake iko Dar es Salaam, hajui anarudije kwa sababu kazi zao zinaenda kwa order, usipompatia hela unataka nini? Mke wake kule atatafuta mtu, atatafuta mbadala na yeye huku atatafuta mbadala. Kwa hiyo, ninaomba walipwe sawa sawa na stahiki yao wanayotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jeshini kulikuwa kuna maduka ambayo yana punguzo la bei, lakini tunaambiwa kwamba yale maduka yamefungwa. Wanajeshi hawa hawana muda wa kufanya biashara, wanahitaji kupata incentives, kumuwekea duka lenye bei nafuu ni kumtia moyo wa utendaji kazi. Sasa sijajua hizo bajeti na jinsi ya kufunga mikanda kama kunafika hadi kwenye Jeshi, tukifika hapo nchi inaangamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kauli zinasemwa na Waheshimiwa Wabunge wengine, sitaki kuwataja umekataza, tunapozungumzia haki sisi sio Wazambia, sisi ni Watanzania, ni wazawa, tunazungumzia mustakabali wa Taifa hili bila kupendelea. Si sawa kutuona sisi ni magaidi tunapozungumzia na kusema tunawachonganisha wanajeshi na wananchi, kwani wanajeshi hawajui kama wao wanakosa haki zao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna haki ya kuzungumza pasipo kupendelea; na msijifiche kwenye kichaka cha kwamba sisi ni wapinzani, tunayo haki, tunalipwa mshahara sawa na ninyi na lazima tulalamike na lazima msimamie haki na muifanye kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Wananchi linajitahidi sana kutetea Taifa letu, lakini ijapokuwa hii inahusika na miundombinu pia, kwenye mipaka yetu madaraja ni mabovu. Leo hii tukipata shida kama nchi mimi nakwambia hivyo vifaru ambavyo wanavyo kwa kupitisha hawana. Sasa hapa Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi uonane na Waziri wa Miundombinu uone ni jinsi gani utaweka mipakani madaraja. Kule kwetu Kyela madaraja ni mabovu, Malawi wameonesha chokochoko kuja kwetu, je, wakifanya kweli, tunapita wapi? Ninaomba unapokuja kuhitimisha ujaribu kuliweka hili wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vijana wanafanya kazi ya ulinzi kwenye SUMA JKT, mishahara wanayopata ni midogo. Sote tunajua kuna makampuni ya ulinzi yanalipa hadi shilingi 500,000 wafanyakazi wao, vijana hawa wanapata chini ya shilingi 200,000, mimi nafikiri si sawa. Ninaomba Mheshimiwa Waziri kwa bajeti inayokuja ufikirie jinsi gani vijana wale wataongezewa mshahara. Na ninaomba pia na ninashauri kama ikiwezekana makampuni binafsi mengine yapunguzwe, ili tuongeze idadi ya vijana kwenye JKT na kuchukua tender, ikiwezekana zote kwenye Serikali, lakini pia hata makampuni binafsi tulazimishe wachukue SUMA JKT. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Wananchi pamoja…
(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia kwanza kuhusu wakulima wa chai Rungwe. Kumekuwa na migogoro mingi sana kati ya wakulima wa chai Mkoa wa Mbeya, Wilaya ya Rungwe na wadau wa chai akiwemo Mohamed Enterprises na WATCO kwani bei ya chai ni ndogo sana na baadhi ya wakulima kujiondoa katika uuzaji wa chai katika viwanda vya Katumba na Busokelo kwa madai ya maslahi madogo na wakati huo huo Bodi kuzuia kuuza kwa chai na kampuni ya Mohamed Enterprises na kuzuia uhuru wa kibiashara ambapo mwisho wa siku mkulima ndiyo hunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili mazao kuuzwa kwa ujazo wa lumbesa. Naomba Wizara iweke mkazo na msisitizo wa kusaidia wakulima wanapouza mazao kulazimishwa kujaza mazao katika mfumo wa lumbesa kwani wakulima hupata hasara kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, naomba niongelee kuhusu pembejeo zisizo bora. Kumekuwa na malalamiko ya pembejeo zisizo na kiwango na kupelekea makusanyo duni na kuwapa hasara wakulima wetu hasa wa Mkoa wa Mbeya. Serikali ina mkakati gani wa kusaidia wakulima hawa na pia kuchukua hatua kwa wahalifu wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, niongelee kuhusu bei ndogo za mazao. Wizara inasaidiaje wakulima wauze mazao yao kwa bei ya faida ambayo itasaidia kulipa gharama za kilimo walichowekeza na kudhibiti madalali wanaopata pesa nyingi kuliko wakulima wenyewe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, Kituo cha Kilimo Uyole. Kituo hiki ni muhimu sana kwa wakulima wa Nyanda za Juu Kusini kwani utaalam wao unahitajika lakini cha kushangaza pesa inayotengwa kwa shughuli za maendeleo haziwafikii kwa wakati na hata wakati mwingine kutofika kabisa na kukwamisha shughuli za kitafiti na kiutendaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita ni kuhusu wakulima na wafugaji. Tunaomba ufumbuzi wa kudumu juu ya wakulima na wafugaji utafutwe ili kupunguza/kuondoa ugomvi kati ya jamii hizi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nami kuweza kuchangia Wizara hii ya Kilimo. Nimesimama kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Mbeya, kila mtu hapa anafahamu Mkoa wa Mbeya ni mkoa ambao unaweza ukalisha nchi hii vizuri lakini bado nashangaa kwa nini Serikali haitaki kuwekeza zaidi katika mkoa huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda hasa kwa kuchambua Mkoa wa Mbeya nitazungumzia Wilaya ya Kyela. Wilaya ya Kyela ina mambo mengi ambayo yanaweza kulisaidia Taifa hili. Tunafahamu Ziwa Nyasa linatoa samaki wa aina nyingi ambapo kama tukiwekeza katika lile ziwa tunaweza tukasafirisha samaki katika nchi yetu wenyewe lakini katika soko la Afrika Mashariki. Tunafahamu Kyela kunapatikana cocoa, Mheshimiwa Waziri anapokuja kuhitimisha hotuba yake atuambie ni nguvu gani amewekeza katika zao la cocoa. Tunajua cocoa inanunulika sana katika soko la dunia lakini mwananchi wa Kyela amefaidikaje na zao hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye mpunga, Wabunge mnafahamu kuna mahali mpaka tunadanganywa mpunga wa Kyela, kwa nini tusiwekeze katika mpunga huu kama unapendwa na una soko zuri kuweza kusaidia wale wakulima wadogo wadogo ambao pia wengi wao ni wanawake tukaweza tukapata zao hilo na faida yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua hii Benki ya Kilimo kwa nini isiende kusaidia wananchi wa Mkoa wa Mbeya. Wananchi wanapolima tatizo kubwa tunaona ni mitaji, twende mahali tuachane na kilimo cha jembe, tunahitaji kilimo cha kibiashara ili kuweza kumkwamua mwananchi katika kujiendeleza maisha yake ya kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la Benki ya Kilimo, najua ipo Dar es Salaam sijui kama ina matawi, kama ina matawi hayafanyi kazi, ukienda huko kwetu Rugwe, Kyela, Mbarali hakuna mwananchi anayeijua na wala hata kupata maelezo ya benki hii ikaweza kuwasaidia hawa wananchi. Naomba Wizara ichukue juhudi za makusudi kusaidia wanawake na wananchi wa Mkoa wa Mbeya waweze kujua maana ya kuwa na Benki ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia pembejeo. Pembejeo imekuwa ni tatizo kubwa sana katika Mkoa wa Mbeya. Kwanza haziji kwa wakati, pili nyingi ni feki, hata hatujaelewa Serikali imechukua hatua gani kwa wale walioleta pembejeo zisizofaa. Naomba kwa bajeti ya mwaka huu pembejeo zifike kwa wakati na zilizo bora kwa sababu hata Wabunge wenzangu wamelalamika mazao hayatoki mengi ni kwa sababu mbegu hizi si bora na hata hizi mbolea zinazokuja si sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara isimamie na ituambie inafanyaje na kama inaweza ikabadilisha mtindo ambao unatumika sasa wa ugawaji wa pembejeo kwa sababu wachache wananufaika na wakulima wanaingia kwenye nafasi ambayo haziwafikii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia suala la chai, nimezungumza mara nyingi katika Bunge lako Tukufu nikilalamika juu ya wakulima wa chai wadogo wanavyolalamika chai isivyowasaidia wao kama wakulima. Ni watu wachache sana wananufaika na zao la chai, mwananchi wa kawaida chai bado iko chini wakati chai inauzwa bei nzuri soko la dunia lakini sisi wenyewe Tanzania tunahitaji kunywa chai kwa nini chai isimnufaishe mkulima wa Mkoa wa Mbeya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia mazao, Mbeya ina mazao mengi sana. Sisi sote tunafahamu unapotaka kupata karoti unapata Mbeya, unapata viazi lakini linakuja tatizo kwenye soko, bei ya mkulima ni ndogo anayefaidika ni mtu wa katikati ambaye ni dalali. Tunawezaje kusaidia wakulima wakauza mazao yao kwa bei ambayo ni nzuri. Mwananchi wa kawaida anahangaika kulima mwisho wa siku anauza gunia la viazi Sh.25,000, Sh.20,000 au Sh.30,000 lakini ukija Dar es Salam gunia hilo hilo linauzwa kwa Sh.150,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali inamsaidiaje mwananchi huyu aweze kuuza kwa bei kubwa na tunajua kabisa mpaka sasa kuna watu wanatoka Kenya wanakuja huku kwenye masoko yetu na mashamba yetu bado wananunua kwa bei ndogo. Tunahitaji wateja waje lakini Serikali inawabanaje wanunue kwa bei inayomnufaisha mkulima wa kawaida?

Tunapozungumzia kilimo tunahitaji kuwekeza kwenye kilimo kweli kweli wala si katika maneno. Tunapozungumzia mpunga, tumezungumzia mpunga wa Kyela ulivyo mzuri lakini tuna Mbarali, Mbarali kuna shamba kubwa sana la mpunga lakini je Serikali imewasaidiaje wale wakulima wa Mbarali, imesaidiaje wale wakulima….

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na Malengo ya Milenia (MDGs) hatukuweza kufikia malengo, tulifanikiwa maeneo matatu tu na hata hivyo UNESCO ilitupatia tuzo katika uandikishaji wa watoto, kwa hilo napongeza japo hatukuweza kuwa na elimu bora kwa watoto wetu japo waliandikishwa kwa wingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu kwa sasa tuna SDGs ambayo malengo yake ni mengi zaidi ya MDSs. Je, katika Mpango huu Serikali imejipangaje kuhakikisha inaingiza katika Mpango huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi yoyote makini, lazima iwe na vipaumbele vichache visivyoweza kushindwa katika utekelezaji, Tanzania kwa sasa ina vipaumbele gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawezaje kuwa na maendeleo na mipango bila kilimo. Viwanda bila kilimo ni uti wa mgongo ni vema tukazingatia kilimo maana viwanda vinategemea malighafi za kilimo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa kama Mjumbe wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, sikitiko langu ni sawasawa na Wajumbe waliopita. Tatizo la bajeti, Bunge tunapitisha lakini mwisho wa siku pesa haziendi kwa wakati kwenye kasma ambayo sisi tumeipelekea. Sasa Mheshimiwa Waziri utakapokuja kujibu hoja yako jioni, ninaomba utuambie safari hii utafanya nini kuhakikisha fedha hizo zinafika kwa wakati hasa zikasaidie kazi za Balozini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tunazungumzia uchumi wa kidiplomasia. Sisi kama Kambi, Mbunge wetu ameelezea vizuri sana ni jinsi gani inabidi tujikite kwenye uchumi wa kidiplomasia. Na mimi nazidi kusisitiza kwamba bila kuwa na uchumi wa kidiplomasia hatuwezi kufanya vizuri kwenye zama hizi za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeingia katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, tunafahamu biashara nyingi sana zinaendelea, lakini kundi kubwa la wanawake ambao ndio wajasiriamali wakubwa, sijaona kama Wizara imefanya juhudi za makusudi kuweza kutambulisha fursa hizo za kijasiriamali kwa wanawake wa Tanzania kwa ujumla wake. Kuna maonesho mbalimbali yanafanyika, likiwemo Jua Kali na mengineyo, sijaona kama Wizara imetangaza hata kwa kutumia Televisheni ya Taifa kuwaeleza wanawake wa Tanzania kuzijua hizo fursa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ni ya muhimu sana. Tunajua kwamba Mabalozi wanalipwa mishahara kule waliko. Wanatumia juhudi gani kuitangaza Tanzania hasa katika maeneo ya kiutalii pamoja na mambo mengine ambayo watu wetu wanaweza wakanufaika na hizo nchi. Nadhani ifike wakati tupeleke wataalam na kama wapo, wapewe onyo kali wasipofanya kazi zao na wajibu wao wa kuitangaza nchi katika hizo nchi wanazokaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, tuna tatizo katika Wizara hii. Balozi mmoja, kwa mfano Balozi wa Msumbiji, anasimamia na Balozi nyingine zinazomzunguka. Ni kweli tunabana bajeti, lakini mwisho wa siku ufanisi unakuwa mdogo kwa sababu hakuna pesa zinazokwenda mahali pale. Kwa hiyo, nashauri bado ninafikiri tuna wasomi wengi katika Taifa hili, ninaomba wapewe nafasi za Ubalozi katika hizo nchi badala ya kutegemea Balozi mmoja kusimamia Balozi zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie Chuo cha Diplomasia, Kurasini. Chuo kile ni cha muhimu sana na wote tunajua kwa nini kilianzishwa. Hivi tunavyoongea kile chuo wenzetu wa Msumbiji walijitoa, lakini pia hatuna pesa ya kukiendeleza kile chuo. Mapato yanayotumwa kwenye kile chuo ni madogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri atakapokuja tunaomba atuambie, tunasimamiaje chuo kile ili kiendelee kutoa Wanadiplomasia makini katika Taifa letu la Tanzania? Tunataka kujua kwa nini wenzetu wa Msumbiji walijitoa na wengineo? Basi watuachie tubadilishe matumizi ya chuo kile kiweze kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie suala la Jumuiya ya Afrika Mashariki na lile jengo letu la AICC pale Arusha. Nataka kujua linasaidiaje? Kwa sababu ninaamini pesa zinazopelekwa bado ni ndogo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ukuaji na uingiaji wa watalii ulikuwa asilimia 12.9 mwaka 2015/2016; mwaka 2016/2017 mwaka wa kwanza wa Awamu ya Tano kasi imeshuka mpaka asilimia 3.5 tu. Hifadhi ya Ruaha inayopakana na wananchi maeneo ya Mbarali wapo katika wakati mgumu wa kufukuzwa kwenye makazi yao na mpaka sasa hakuna hata waliopata fidia yoyote mpaka sasa hawana cha kufanya.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ukataji wa miti kilometa za mraba 1,430 sawa na zaidi ya ukubwa mkoa mzima wa Dar es Salaam huu mradi si wa Watanzania kwa maana ya kuwasaidia. Tunaomba Serikali ichunguze na kuamua kwa faida ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, Guanzhuo ni mji wa kibiashara lakini hatuna Balozi Mdogo na timu ya kutangaza biashara hasa watalii kuja nchini kwetu kwani Kenya ina timu inayofanya matangazo ya nchi yao. Hakuna pesa za kutangaza utalii kwa nchi yetu na kutegemea makampuni binafsi ambayo hata wao hawaweki mkazo juu ya utalii huu. Vifaa vya kutendea kazi kwa wafanyakazi mbugani kama magari, tochi, bunduki hata boti sehemu zenye kuhitaji mabomu. Tunaomba Serikali iongeze bidii katika kuwezesha fedha za utendaji.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Rungwe kuna vivutio vingi sana lakini hakuna uwekezaji wa kutosha ili kuvuta watalii maeneo hayo ni Daraja la Mungu, Lake Ngozi na Kijungu. Haya maeneo ni ya muhimu sana kwa uchumi wa Wilaya ya Rungwe tunaomba Serikali iwekeze maeneo hayo.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, nianze na suala la upelekaji fedha Wizarani kwa ajili ya miradi. Kutotoa pesa za mradi kwa wakati ni changamoto kubwa sana kwa asilimia tano kwenye miradi mbalimbali na kupelekea kuzorotesha miradi ya maendeleo. Nikichukulia Wizara ya Mambo ya Ndani kazi nyingi zimeishia njiani na kupelekea kupoteza fedha nyingi zilizokwishatumika katika miradi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu fedha shilingi trilioni 1.5; mnamo mwaka huu kulitoka report ya mkanganyiko ya mwaka 2016/2017 kuna hoja ya shilingi bilioni 203.9 ya Serikali Kuu ya Tanzania kwamba ulikusanya kwa niaba ya SMZ, hii si kweli kwani SMZ mwaka 2016/2017 bajeti yao ilikuwa shilingi bilioni 841 na kati ya hizo shilingi bilioni 452 ni vyanzo vya ndani na nje na shilingi bilioni 58.9 katika mapato ya ndani, mapato ya kodi yalikuwa shilingi bilioni 366.0; makusanyo ya ZRB na TRA na mapato yasiyo ya kodi shilingi bilioni 23.6. Shilingi trilioni 1.5 ni karibu mara mbili ya bajeti yote ya Zanzibar. Naomba kujua zipo wapi?

Mheshimiwa Spika, Wizara imeonesha udhaifu kusimamia Deni la Taifa kwa kuwa deni limezidi kuongezeka na kuwa na athari za kitaifa; mid-year review katika mwaka 2017/2018 iliyotoka mwaka huu Februari, 2018 ni kwamba Deni la Taifa liliongezeka kwa dola 1,054.6, sawa na shilingi trilioni mbili, bilioni mia tatu na milioni mia moja ishirini. Deni limefikia trilioni hamsini na tisa, bilioni thelathini na saba. Ni shida kwa Taifa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. SOPHIA. H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii. Kwanza kabisa nitazungumzia utawala bora kama wenzangu walivyosema. CAG mara nyingi alikuwa akitoa ripoti na ripoti zake nyingi sana zimeeleza ubadhirifu wa mali uliofanywa na Serikali ya CCM. Ninachotaka kushangaa kuna msemaji aliyepita amezungumzia habari ya Chama cha CHADEMA lakini nikaona huyu mwenzangu labda hajasoma kitabu chote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zetu wa Chama cha Mapinduzi wamechukua pesa za watu ambao walitakiwa walipwe pension kwa cheque number 156424 wakazitumia vibaya. Mpaka CAG anakagua hesabu mwezi wa Pili hizo pesa hazijarudishwa. Anazungumzia tujitoe boriti kwenye jicho letu, huwezi kuwa nyoka ukazaa mjusi. Ili uweze kuwa safi pia lazima uzae mtoto safi, makosa ni ya CCM, si ya CHADEMA.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia utawala bora wewe kama kweli ni chama tawala na uko vizuri na unafanya kazi sawasawa na ilani ya chama chako kwa nini unatumia nguvu ya kuzuia upinzani ambao tayari ulipita kihalali na uliusaini na ukakubalika? Huwezi kuwa mzazi, watoto wawili wanagombana mmoja umemshika mkono halafu unajiita wewe ni mshindi, hiyo siyo kweli. Tupewe uwanja sawa, twende viwanjani na sisi tukazungumze, tuone zile kule milioni sita feki mlizotupa kama hatujawapiga 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye Wizara sasa, maana na mimi nilikuwa najibu ndugu aliyezungumza. Soko la Kariakoo lilijengwa kwa makusudi ya kusaidia wakulima na kuuza vifaa na pembejeo kwa ajili ya wananchi. Najua ni miaka mingi imepita soko lile kuwa pale, lakini tuna Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini inayozalisha mazao mengi; huu ni wakati sasa mngejenga masoko hayo kwa ajili ya kuwasaidia wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri, Mkoa wa Mbeya ni mkoa ambao uko katikati, una mazao mengi sana, tunashauri mtupatie masoko ya kimataifa yanayoweza kusaidia wanawake ambao wanalima kwa nguvu zao zote waweze kupata masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejiunga na Afrika Mashariki lakini cha kushangaza wenzetu wa Kenya, Waganda wanakuja hadi vijijini kununua maparachichi bila utaratibu unaokubalika. Tukiwa na masoko haya tunaweza tukafanya kazi nzuri na tukasaidia uchumi wa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nazungumzia habari ya masoko hayo hayo. Leo hii Mheshimiwa Jafo, Tunduma wamefunga masoko; sijaelewa wanaposema ninyi mnatetea wanyonge, mmepoteza hela ngapi kwa siku ya leo kufunga soko la Tunduma? Sijajua ni kwa nini tunawaachia Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa waamue mambo bila kutumia utaratibu na professionalism?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Mheshimiwa Waziri kama kiongozi wa Wizara hiyo, tunaomba Soko la Tunduma lifunguliwe. Tunadaiwa madeni mengi, kwa sababu mwishowe wafanyabiashara wamesema wanatupeleka mahakamani; ni nani atalipa pesa hizo? Halmashauri hii wameifungia Madiwani, kazi haziendi kisa Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya. Hapa ndipo ninapoushangaa huu utawala bora Mzee Mkuchika. Naomba ninyi wazee ambao bado mpo na mpo kwenye system shaurini Serikali ifanye kazi sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija upande wa mikopo, ilitengwa bilioni sitini na moja kwa ajili ya wanawake na vijana, lakini bilioni kumi na tano ndizo zilizotumika. Idadi ya wanawake ni wengi lakini pesa zilizotoka ni kidogo. Tunaomba waachilie vyanzo vya mapato kwenye halmashauri ili tuweze kukusanya pesa nyingi na kusaidia wanawake na vjiana kwa ajili ya ahadi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo ugawaji wa mikopo hii unakwenda kiitikadi… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru pia kuwa mmoja wa wachangiaji wa bajeti hii. Binafsi naunga mkono bajeti ya Kambi Rasmi ya Upinzani iliyozuiliwa kusomwa hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu wake kama tulivyosema bajeti hii ni ya kufikirika na sidhani kama itatekelezeka. Kwanza kabisa Deni la Taifa. Wizara hii ndiyo msimamizi mkuu wa Deni la Taifa na mali za nchi. Toka awamu hii imeingia madarakani Deni la Taifa limeongezeka kwa kasi kubwa sana na yeye kama kiongozi anayehusika haoni kama analiletea Taifa hili changamoto inayotusubiri hapo mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwezi ameji-commit na Wizara yake kulipa Deni la Taifa shilingi bilioni 883. Ameji- commit na ana wajibu wa kulipa mishahara ya watumishi karibu shilingi bilioni 617 na kuendelea. Wakati huohuo kuna OC shilingi bilioni 254. Mapato, tukiachia mnavyo-forge maana mmeeleza mapato ni mengi wakati uhalisia si kweli. Matumizi ni 1.7 lakini mapato ni 1.2, hizi nyingine anapata wapi? Kwa hiyo, namsisitiza kwa faida ya Watanzania na hasa wanawake ninaowawakilisha namwomba awe realistic, asiweke figure za kufurahisha viongozi au baraza lake, ahakikishe anaweka figure ambazo zitawasaidia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, naona niache habari ya Deni la Taifa kwa sababu ni cancer ya Taifa. Nataka niingie kwenye habari ya kilimo. Toka tunapata uhuru tulikuwa tunasema kilimo ni uti wa mgongo na kilimo kinachukua zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania, bajeti ya 2016/2017

T A A R I F A . . .

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, mama ni yake wa kambo, kwa hiyo, naelewa anachofanya. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nachotaka kusema ni kwamba 2016/2017 tuliweka bajeti ya shilingi bilioni 1.1 kwa ajili ya bajeti ya kilimo lakini ni shilingi bilioni 3 tu ndiyo zilitoka. Kama unazungumzia kilimo ni uti wa mgongo na sisi kama Bunge tulipitisha hizo pesa tukijua hata kama hazitoshi zinaweza zikasaidia lakini ikatoka shilingi bilioni 3 peke yake. Mwaka huu tunaoumaliza sasa tulitenga shilingi bilioni 150 lakini mpaka leo zimetoka shilingi bilioni 27 peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo ndiyo kila kitu na wewe mwenyewe umetoka kwa wakulima unafahamu, kama pesa haijatoka na sisi Bunge tumepitisha, sioni umuhimu wa kuwepo mahali hapa unless tunafanya siasa. Bunge kama chombo muhimu kimesema pesa kadhaa itoke Wizara haijatoa na wanajinasibu wanakusanya pesa nyingi, sielewi wanasimamia mpango gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kutoa pesa ndogo kwenye kilimo bado kilimo kinaingiza kwenye pato la Taifa takribani asilimia 30 ya pato la Taifa. Kwa nini kama Watanzania tusione umuhimu wa kuwekeza zaidi kwenye kilimo pamoja na viwanda tunavyovizungumzia tukaweza kupata pesa nyingi isiyokuwa na matatizo. Leo hii tuna Vyuo vya Kilimo, kwa mfano, SUA na Uyole huu ni mwaka wa tatu hawajapata pesa za utafiti. Unawezaje kuwa na kilimo safi hufanyi utafiti?

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumza kilimo, tunazungumzia mbegu bora, jana kuna mmoja ametoka kuuliza swali juu ya mbegu za alizeti, mkulima kwa gharama yake anapanda mbegu lakini mbegu haioti. Watafiti hawawezi kusema lolote kwa sababu hawajapewa pesa kwa ajili ya utafiti. Leo hii kuna mbegu za mahindi zinapandwa, hakuna chochote kinafanyika kwa sababu hizo mbegu si mbegu bora lakini hatuwezi kuwalaumu watafiti wetu kwa sababu hawana fedha ya utafiti. Tukienda kwenye mambo hayo hayo ya kilimo, katikati ya kilimo kuna mitamba ile inayotakiwa kufanyiwa utafiti hawajapata pesa. Pale SUA Arusha hawajapata pesa kwa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazungumzia habari ya kilimo ambacho kimebeba idadi kubwa sana ya Watanzania na mimi ninayewakilisha Mkoa wa Mbeya asilimia kubwa wewe ni shahidi, wanawake ndiyo wanaoingia kwenye kilimo. Kwa gharama zao wenyewe wanaamua kulima, hawana Maafisa Ugani, wako wachache, hawana maelekezo yoyote mwisho wa siku wameshalima lakini masoko pia hamna. Tumeingia kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki wenzetu wamejipanga kwa nini na sisi tusiige, kwa kweli masoko ni shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi nikisimama hapa nazungumzia suala la chai. Mpaka sasa hatuna viwanda vidogo vidogo vya kusaidia wakulima hawa. Hatuna mkakati wa mbolea au kuwasaidia kwa namna yoyote kama Taifa lakini bajeti inayotengwa ni ndogo na hata hiyo ndogo inayotengwa Wizara haitoi pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii bajeti sijajua walifikiria nini au kuna kitu gani wanakifanya? Hali ya hewa huwezi kuitegemea kwenye kilimo. Tanzania tunaishi kwa kutegemea Mungu anasema nini kwa ajili ya kutuletea mvua. Hatujajipanga kwenye umwagiliaji, hatujajipanga kuhifadhi maji ya mvua, tunasubiri Mungu atoe na asipotoa hatuna kilimo. Naomba sana Mheshimiwa Dkt. Mpango tulitazame suala hili kwa upya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niende kwenye eneo la wafanyakazi. Sasa hivi imeletwa sheria ya ufutwaji wa Tume ya Mipango. Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango alikuwepo toka awamu iliyopita kwenye Idara hiyo, Marais karibu wanne wamepita hakuna aliyethubutu kufuta hii Idara lakini wanafanya hivyo kwa sababu wanataka wawe huru na kufanya wanavyotaka. Hawataki kuwa na chombo cha kuwasimamia, wanachota hela Bombardier, Chato, hawataki usimamizi. Kwa sababu tukiwa na hii Idara sisi tutaiuliza lakini wanaiondoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mfuko mmoja wa mapato ya Serikali wanataka ubadilishwe sijajua wanawaza nini. Hatuwezi kumlazimisha maana ameshika mpinina sisi tumeshika makali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uhakiki wa wafanyakazi umekuwa kwa muda mrefu, kuna sehemu umemalizika lakini kuna watu walipandishwa madaraja miaka miwili iliyopita hawakulipwa mishahara yao. Umefika wakati wa kulipa mishahara yao sawasawa na madaraja waliyopanda
mnawaambia waandike barua kwa wakati mliosema kwa maana miaka ile mingine inapita bila wao kupewa haki yao, huu ni dhuluma na hii ni dhambi mnaipanda kwenye Taifa hili. Jasho la mtu likipotea, kuna wakati hata tunapeleka watoto wetu shule hawafaulu mitihani kumbe ni pesa ya laana. Umempeleka mtoto shule unalipa ada kumbe ile ada uliyolipa kuna watu wanalalamika mahali fulani. Namuonya Mhesimiwa Dkt. Mpango naomba atetee hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye viwanda, nitazungumzia upande wa Kiwanda cha Ngozi. Hatuna kiwanda cha ngozi na ng’ombe wanagongwa alama tayari hiyo ngozi yao haina thamani. Ng’ombe wanatembea kilometa nyingi, hiyo ngozi haina thamani. Nashauri kuwawekea wafugaji maeneo mazuri ya kulima na kutunza mifugo hiyo ili tupate thamani ya ngozi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda anavyovizungumza Mheshimiwa Mwijage, cherehani tatu anaita ni kiwanda, huku ni kuwachezea Watanzania. Namshauri kaka yangu asifanye vitu kisiasa. Mnapokuwa kwenye cabinet, Mheshimiwa Mwijage nakuamini, shauri hali halisi. Mimi nimegawa vyerehani zaidi ya 400, anataka kuniambia mimi ni mfadhili wa viwanda? Hiyo si sawa. We need the real project, hatuhitaji kufanya vitu kisiasa, kuwanufaisha Watanzania. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la afya ni tatizo hasa kwa magonjwa yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii. Kabla ya yote, nataka nimpongeze Mwenyekiti wetu na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani pamoja na viongozi wa CHADEMA ambao kwa sasa wako katika kadhia ya kuripoti Polisi kila Ijumaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka nizungumzie suala la Zimamoto. Zimamoto mwaka 2016/2017, Bunge lilitenga pesa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kununua magari mawili ya Zimamoto, lakini pesa hizo hazikuweza kutoka sawasawa na Bunge lilivyopitisha. Tender Board ilikaa wakazungumza na Wizara ya Fedha pesa ziweze kutoka, zilitoka shilingi milioni 117 peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia viwanda, viwanda na moto ni vitu vinaenda pamoja. Kama hutaweza kutenga pesa kwa ajili ya magari ya Zimamoto unakuwa hujafanya sawasawa katika utekelezaji wa kuleta maendeleo. Mwaka 2017/2018 Serikali ilitenga shilingi bilioni 3.5, haikutoka hata senti tano kwa ajili ya watu wa Zimamoto. Jeshi hili ninavyoliona ni kama Jeshi ambalo limesahaulika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unafahamu kabisa kwamba Jeshi hili hata ukiangalia mavazi yao, ni chakavu kuliko majeshi mengine. Sasa sijajua tunawaweka katika ma-grade kwa sababu gani? Kwa hiyo, naomba Serikali na namwomba Mheshimiwa Waziri anapokuja kujibu hoja, tunataka kujua hizi pesa tunazopitisha kama Bunge, halafu hazitumiki na wala hazitoki, Wizara ya Fedha haitoi pesa. Kama Bunge limepitisha, kwa nini Wizara haitoi? Namwomba Mheshimiwa Waziri aje atoe majibu anapokuja kuhitimisha hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia jengo la Mchicha. Unajua Zimamoto mpaka sasa hivi wanapanga na kuna jengo tayari Serikali imeshaweka pesa pale, jengo halijakwisha, limechakaa na safari hii hakuna hata senti tano iliyotengwa kwa ajili ya jengo lile. Sijajua tunawaza nini na tunafikiria nini kwa ile pesa tuliyoizamisha pale Mchicha, mpaka leo hiyo pesa hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Jeshi la Polisi. Jeshi la Polisi kuna wakati niliwahi kuongea na IGP nikamwambia kwamba Jeshi linafanya kwa professionalism. Unapokuwa na jeshi lazima na intelijensia inafanya kazi yake kwa makini kwa kufuata weledi wa kile walichosomea. Leo hii Jeshi la Polisi linafanya kazi na mitandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, binti mdogo anaitwa Mange Kimambi anaanzisha maandamano mtandaoni, leo wanalitoa Jeshi sehemu za siri kulileta barabarani. Sidhani kama wako sahihi. Wakitokea Mange Kimambi 10, wanataka kuniambia watashinda wakifanya mazoezi barabarani? Sidhani kama wako sahihi. Mheshimiwa IGP, nafikiri inabidi kujitafakari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri Mwigulu alipokuwa Singida sikumbuki ilikuwa hafla gani, alizungumzia kuhusu waandamanaji na akasema waandamanaji watakapoandamana inaweza ikatokea kupigwa risasi. Sasa sijajua kwamba anaota au sijajua kama yeye ni Mfalme Njozi, sijafahamu. Ninachojua, Polisi kazi yake ni kulinda raia. Maandamano mimi naona wanazungumzia kama ni dhambi au kitu kibaya. Jeshi la Polisi kazi yake kufanya intelijensia. Elimu waliyosomea ipo kwa ajili ya kuzuia mabaya, wala haipo kwa ajili ya kutetea kwa kutumia vitu vya kufikirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwa Waziri, Mheshimiwa Mwigulu, yeye ni kiongozi wa wote. Hisia zake za kichama ajitahidi kuzidhibiti zisiweze kumtoa kwenye reli. Naomba afanye kwa weledi, ataacha alama katika jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapolalamika, Polisi wanaposema wamefanya utafiti na kugundua kuwa kutatokea hali mbaya, sijaelewa huwa inaangalia upande mmoja, au ni pande zote. Kiongozi wa Chama cha Upinzani, kiongozi wa Jimbo kwa maana ya Mbunge, anaandika barua ya kufanya Mkutano ambao huo wameuruhusu, lakini Polisi inatoa majibu ndani ya masaa mawili kabla ya Mkutano kusema kwamba tumegundua amani haitakuwapo. Kwa kweli nashindwa kuelewa. Mikutano hii akifanya Polepole intelijensia haioni ubaya, lakini akifanya mtu wa CHADEMA Mheshimiwa Heche, intelijensia inaona ubaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu, nataka kuwaambia, siku zote ubaya wa kidogo kidogo huwa unajenga chuki ndani ya watu. Mheshimiwa Bwege mchana wa leo amezungumza na mkamshutumu kwamba anaongea kwa hisia, lakini kumbukeni mabaya huwa hayatokei isipokuwa yamefanywa kidogo kidogo mwisho wa siku yakawa makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa hili ni la wote na wala siyo favour sisi kuwepo hapa. Ni haki yetu na wajibu wetu na kwa sababu walikubali vyama vingi, wakubali kumeza vidonge vya vyama vingi. Polisi watuachie CCM tukae nayo pembeni sisi wenyewe tufanye nao siasa, wao wakae pembeni. Kwetu sisi CCM ni wepesi kama karatasi wakikaa pembeni; lakini wakitulazimisha na sisi ni binadamu, tutatafuta njia mbadala ili kuhakikisha tunafikia wapi tufike kwenye malengo tunayoyataka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia Uhamiaji, dada yangu kiongozi wa Uhamiaji anafanya kazi vizuri, lakini bado kuna maeneo madogo madogo hasa kwenye biashara ya kujenga nyumba za Uhamiaji, asimamie vizuri pesa za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye Jeshi la Magereza, wako vizuri, wanafanya vizuri. Tatizo lao Magereza pia ni kama la Zimamoto kutokuwa na vifaa vya kutosha ikiwemo nyumba za kuishi, lakini uniform ni kilio kikubwa sana kwa wafanyakazi hao. Magari kwa Magereza ni shida. Ukienda mikoani, wanahitaji kupeleka wafungwa kwenye kesi, hawana magari. Sasa sijajua tunategemea nini? Kesi zitaendaje? Watafanyaje kama hatutaliwezesha jeshi hili kufanya kazi zao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kwamba uhalifu umeongezeka kama wanavyosema, lakini Magereza mengi yana vyumba vidogo. Magereza mengi hayana vyumba vya mahabusu vya wanawake. Wanawake kwa mfano ukienda Gereza la Kyela, hakuna sehemu ya kuweka wanawake, wanaenda kulala Tukuyu. Ni mwendo mrefu sana na wakati huo huo hawana gari la kuchukua hao watuhumiwa na kuweza kuwapeleka Tukuyu na Kyela. Naomba Mheshimiwa Waziri anapokuja atuambie amejipanga vipi kuondoa changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado nafikiria sisi kama Bunge hatujajipanga sawasawa kuisimamia Serikali. Ni mara nyingi tumepitisha bajeti lakini bajeti hizi hazitoki. Bajeti hizi, pesa hazitoki, ni hadithi. Watu wetu wanakuja hapa Dodoma, tunakaa nao, tunawasikiliza kwenye Kamati, tunakubaliana. Ikifika kwenye utekelezaji, hiyo imekuwa ni shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Bunge lako Tukufu linapopitisha bajeti, tunataka tukija kwenye mwaka mwingine wa fedha hizo pesa zifanye kazi na ziwasaidie watu wetu kufanya kazi zao na waweze kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naomba kuunga mkono Kambi Rasmi ya Upinzani, najua hatujaleta maoni yetu, lakini bado tunaamini kwamba maoni yetu yangali yanaishi hata yale ya mwaka 2017 yanaweza kuendelea kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nashukuru. Ahsanteni.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi naomba niunge mkono Kambi Rasmi ya Upinzani maana na sisi tumetoa dira, mwelekeo na mpango ambao tunafikiri Serikali mnaweza mkaufuata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwanza nataka nizungumzie kilimo. Tunapozungumzia kilimo ambayo tukimechukua asilimia takribani 75 ya Watanzania wamejikita katika kilimo, lakini katika mpango huu ambao Mheshimiwa Mpango umeuleta hatuoni nguvu ya Serikali kusaidia wakulima wa Tanzania waweze kukuza uchumi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ambazo tumekuwa tukipanga Wizara inatoa asilimia mbili tu ya mapato kusaidia wakulima. Tunafahamu kwamba katika kilimo usipoweka pesa wewe kama Serikali na ukitegemea wafadhili wakupatie pesa kwa ajili ya kilimo na bahati mbaya sana wafadhili wenyewe mmeanza kuwakorofisha. EU iliahidi kutoa hela zaidi ya bilioni 200 kwa ajili ya kusaidia kilimo tayari tumeanza kukorofishana nao sijui tutafika wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo kwa Nyanda za Juu Kusini niachilie mikoa mingine hakuna dalili zozote za kusaidia hasa katika tafiti ili uwe na kilimo bora kwanza kabisa lazima ufanye tafiti. Mwalimu Nyerere alijitahidi kuweka vyuo mbalimbali vya kilimo ikiwemo Chuo cha Uyole mpaka sasa zaidi ya miaka mitano hawajawahi kupata pesa za maendeleo kwa ajili ya chuo kile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna viwanda vingi vilianzishwa ili viweze kusaidia wakulima kwa mfano ZZK walikuwa wakitengeneza zana za kilimo ikawa rahisi kuwafikia wananchi kwa ngazi ya chini, leo hii kila kitu tunatoa nje, tunatoa China kwa gharama za kigeni kuweza kuwafikia wakulima mwisho wa siku pembejeo zinakuwa ni bei kubwa sana kuwafikia wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbegu ambazo ndio zinatakiwa zizalishe chakula cha Watanzania asilimia 90 ya mbegu tunaagiza kutoka nje. Bahati mbaya sana mbegu nyingine zimekuwa sio rafiki kwa ardhi ya kitanzania ndio maana ninarudi nyuma kwamba tunahitaji kuwa na watu wanaofanya research ambao watajua mbegu hii inafaa kwa ardhi hii au zao hili linafaa mkoa fulani na watu hawa waweze kusaidia wakulima waweze kupata mazao yanayostahiki.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia connection ya Wizara tofauti ili kuweza kusaidia Wizara mama kuwa na mafanikio sisi kama watanzania tumeshindwa. Leo hii watu wanaohusika na mambo ya hali ya hewa hawawezi kufanya kazi kwa karibu sana na Wizara ya Kilimo kuweza kujua mwaka huu tunalima mazao kadhaa kwa kupata taarifa kutoka kwa wataalam, kila mtu anafanya kazi anavyoona yeye inafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Maji na Wizara ya Kilimo; maji na kilimo vinaenda sambamba, lakini wasipofanya kazi kwa pamoja Wizara ya Maji haina pesa, Wizara ya Kilimo haina watafiti, tunawezaje kufanikiwa katika kilimo na tunawezaje kuwa na maendeleo ya kiuchumi kama Watanzania na kuwafanya wakulima wanapata mazao kwa wakati sawasawa na ubora tunaoutaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na mashirika mbalimbali yakisaidia upatikanaji wa mbegu. Kama mnakumbuka Ukiliguru zamani walikuwa wanashughulika na mambo ya mbegu, sasa hivi watu kama wale wako wapi? CCM mlikuwa na kitu kinaitwa SUKITA kiko wapi? Vitu mbalimbali vilikuwepo zamani kwa ajili ya kusaidia wakulima hawapo, havipo na wala hakuna ubunifu wa kuanzisha vitu vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie habari ya utawala bora na ukuaji wa uchumi. Usipokuwa na utawala bora na umoja na wananchi kutoka ngazi ya chini mpaka Taifa mnakosa nguvu na moyo wa watanzania kufanya kazi ili kuweza kuleta maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi wamezungumza mahali hapa kuhusu Katiba Mpya na hii ipo katika mpango ambao sisi tumekuwa tukiuzungumzia. Huwezi kuwa na maendeleo yoyote kama hamjajiwekea utaratibu wa utawala. Watu walitoa pesa (kodi) tukaweka Tume, wakazunguka nchi nzima, wakaweka utaratibu wa kuweza kuona kama Watanzania tunaishije, leo hii tumeacha na kuishia pembeni, kwa maana pesa zote zilizotengwa zimekwishakupotea ambayo ilikuwa ni kodi ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba utakaporudi utueleze umepanga nini na ni kwa nini Serikali yako inakataa kuzungumzia Katiba Mpya ili twende kwenye mustakabali wa maendeleo yetu hapo baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ulinzi na usalama ni kitu cha muhimu sana katika Taifa letu la Tanzania. Usipokuwa na ulinzi na usalama wawekezaji wanaondoka. Tumekuwa tukisikia mambo mengi yakitokea na sisi kama wananchi na hata kama Wabunge hatujapata taarifa ya kueleza kwa nini wawekezaji wanatekwa na wanafukuzwa na kama wamekosea je, mmefanya njia gani mbadala mpya ya kuweza kuwatangazia utaratibu mpya wa kuwekeza ili watu wasiwe na mashaka na ulinzi wa Tanzania na usalama wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pasipo na usalama hakuna mtu atakuwa tayari kuja kujiunga na Watanzania. Tupo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, watu wanaona ni bora wahamishe bidhaa zao kwenda Kenya, Uganda na sehemu zingine kuliko kuja sehemu ambayo haina uhakika wa ulinzi wa maisha, mali na mitaji yao watakayowekeza. Tunaomba unapokuja kutueleza Mheshimiwa Mpango ueleze Watanzania pamoja na sisi Wabunge ni mkakati gani umejiwekea wa usalama wa wawekezaji; utatumia njia gani ya kuwalinda hata hao wachache waliobaki waendelee kutumika katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda sana kutoa ushauri, vitu vingi sana vinavyofanyika sasa ambavyo vinaharibu kabisa umoja wetu na hasa katika maandalizi ya kutetea uchumi wa Taifa letu. Mimi ninaomba usimamie TRA ambao ni wakusanyaji wa kodi kwa kweli wamekuwa kama ni askari, hawana umoja na wafanyabiashara na sasa hivi imefika mahali hata wenye mitaji ya 300,000 wanahitaji kulipa kodi, ni kweli sikatai kwamba wasilipe kodi lakini lazima zitungwe sheria ambazo zinasaidiana kuweza kuwasaidia hawa watu wajione wana wajibu wa kufanya hiyo kazi ya kukusanya kodi pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na hali ya udhalilishaji mkubwa sana kwa wafanyabiashara na kumekuwa na matamko mengi hasa Wakuu wa Wilaya kufungia makoso kwa sababu za kisiasa. Wakati mwingine tuliona pale Tunduma, muda mrefu sana masoko yamefungwa, zile pesa ambazo siku ile hazikuingia Serikali ilikosa mapato sababu ya siasa. Vivyo hivyo Mbeya soko la SIDO lilifungwa kwa muda mrefu kwa sababu za kisiasa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami nashukuru kupata muda wa kuchangia Wizara hizi mbili, kwanza kabisa nitaanza kuzungumzia TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya asilimia 60 ya fedha za elimu zinaenda katika Wizara hii ya TAMISEMI na hasa kwa ajili ya majengo na infrastructure zote za mambo yanayohusu elimu. Sisi sote tunafahamu TAMISEMI inashughulika na elimu ya msingi na sekondari na hapo ndiyo kwenye msingi hasa wa kutengeneza Taifa la kesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti ya CAG ya mwaka 2016/2017, inaonesha mapungufu yaliyopo katika Wizara ya TAMISEMI ambapo asilimia 85 ni madara, asilimia 52 ni upungufu wa madawati, asilimia 86 ni vyoo na mashimo na matundu lakini asilimia 88 ni kwa ajili ya mabweni. Tunapozungumzia infrastructure kwa ajili ya elimu ya watoto wetu wa msingi na sekondari, ni lazima kama Wizara ijipange upya na kujua kwamba watoto hawa ambao tunawatengeneza kuwa Taifa zuri la kesho tuwawekee mazingira mazuri ya kuweza kujisomea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa bajeti tunayopitisha sisi Wabunge, ndugu zetu wa TAMISEMI hawapati zote. Naomba Serikali wanavyokuja kujibu waniambie kwa nini bajeti haiendi yote maana tunapopanga bajeti sisi kama Wabunge, tunataka kusaidia jamii na hasa wananchi tunaowaongoza waweze kufikia malengo tuliyoyakusudia. Kwa hiyo, natoa ushauri kwa Wizara na Serikali pia, tunahitaji asilimia 25 zaidi ya bajeti iliyopangwa ili iweze kukidhi mahitaji yanayohitajika katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za msingi zina upungufu, na hii natoa kwenye ripoti ya CAG ya mwaka 2016/ 2017. Katika shule za msingi kuna upungufu wa madarasa zaidi ya 85,000. Hii ni idadi kubwa sana kwa nchi yenye watu wengi kama Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2018, Serikali kupitia Waziri wa TAMISEMI, aliahidi kujenga madarasa mapya 10,140 lakini mpaka leo hakijafanyika chochote. Serikali inapoahidi na ilizungumzia kwamba itatoa zaidi ya shilingi bilioni 29 lakini mpaka leo hazijatolewa. Tunajua kweli tunanunua ndege na vitu vingine lakini usipowapa elimu watoto wako na tayari tuko kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki, ushindani wa ajira utakuwa mgumu sana miaka mitano au kumi ijayo. Ndiyo hapo tunakuja kusema lazima tuwe na mipango ya muda mrefu kwa ajli ya kusaidia kizazi chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejaribu kuainisha vitu muhimu na vipaumbele kama Taifa tunavyotakiwa kuvifanya. Kwanza lazima bajeti iongezwe na mazingira ya kujisomea lazima yawe mazuri. Walimu ambao wao ndiyo wanaosimamia hawa watoto, muda mrefu hawajapandishwa madaraja, mishahara haijaongezwa, tusitegemee hawa watu watafanya kazi kwa bidii na kwa ubunifu. Sote tunafahamu mwalimu anayefundisha mtoto wa darasa la 1 mpaka 5, ni lazima awe mwalimu anayejitolea na kujituma na kufanya kazi kwa uaminifu ili kujenga msingi wa mtoto mdogo. Sisi Wabunge hapa wengi tunapeleka watoto wetu kwenye shule ambazo zinalipa vizuri labda ndiyo maana hatuoni uchungu kwa ajili ya watoto ambao wako chini na wanasoma bila kuwa na mpangilio mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tuongeze ajira kwa walimu, uwiano wa watoto na walimu ni tofauti. Mwalimu mmoja shule standard watoto 30 - 35, naijua Shule ya Msingi Majimatitu ina watoto 200 mwalimu mmoja, hiyo siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ni muhimu kuweka uwazi wa Wizara katika programu na mipango mbalimbali endelevu kwa ajili ya kusaidia watoto wetu. Tunaomba Wizara husika itafute wadau iweze kujifunza, pamoja na kukataa takwimu ambazo sisi Bunge tulikataa lakini bado tunahitaji wadau watupe hali halisi ya takwimu kule chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye elimu tulizungumzia habari ya kuondolewa kwa VAT katika taulo za kike Bunge lililopita. Hakuna utekelezaji uliofanyika wa kupunguza bei kwenye taulo za kike. Tunaiomba Wizara aidha, irudi nyuma tena, irudishe VAT lakini itamkwe kwamba tunatoa VAT kwa wale wanaopeleka taulo za kike kwenye shule za msingi na sekondari tu, vinginevyo tumewapa faida wafanyabiashara ambao wameendelea na lile punguzo la tozo ya VAT lakini wakati huo huo watoto wetu hawapati huo msaada wa taulo za kike. Tunaomba Serikali na hasa Wizara ya TAMISEMI isimamie suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie posho za Wenyeviti wa Serikali za Mitaa pamoja na Madiwani. Hawa watu ndiyo wanakaa na wananchi chini zaidi kuliko sisi Wabunge lakini posho zao, mpaka sasa kuna baadhi ya Halmashauri zimekopa, Madiwani hawajalipwa vikao mbalimbali, ikiwemo na viongozi wetu wa vitongoji na vijiji na Serikali za Mitaa. Tusitegemee ufanisi wa kazi kama hatuwezi kuwalipa, sisi Wabunge maslahi yetu tunayapigania na yanafanikiwa. Tunaomba pia Serikali muwatazame watu hawa muweze kuongeza posho na mishahara yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye suala la utawala bora. Tatizo la viongozi sisi Watanzania, tunafikiri tuonavyo sisi ndivyo ambavyo na watu wa kawaida wanaona. Watanzania wa leo siyo wa jana, watu wa Tanzania wanaona, tuna teknolojia, watu wanaangalia simu nchi nyingine wanafanyaje. Leo hii mkutano wa Chama cha Upinzani unazuiliwa, mita 15 kutoka kwenye huo ukumbi unaozuiwa watu wa CCM wanafanya mkutano, tusijenge chuki zisizokuwa na maana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, michezo ya ngumi. Michezo hii ni muhimu sana kwa uchumi wa vijana wa Tanzania lakini kuna shida ya mapromota wengi wanatumia nafasi zao vibaya kwa kupeleka wachezaji nje ya nchi na kuingia mikataba mibovu. Hata hivyo, naishukuru Serikali kwa kuunda Kamati ya Ngumi ambayo kwa muda mfupi imeleta mafanikio kuonyesha mwanzo mzuri.

Mheshimiwa Spika, ulingo. Tunaomba Serikali inunue ulingo mwingine ili kuongeza upana wa matumizi ya ulingo kwani kwa sasa upo mmoja tu.

Mheshimiwa Spika, mabondia wa kike. Tunaomba Serikali isaidie mabondia wa kike katika kuwasimamia kupata haki zao za kikatiba.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niongelee kuhusu mikopo ya vyuo. Vyuo vingi viliahidi utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa masomo ya sayansi hasa udaktari kwa kupata mikopo asilimia 100 lakini wanafunzi wengi hasa wasichana wameacha kozi au kubadilisha kwa ukosefu wa ada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, majengo ya shule za zamani. Majengo mengi yamechakaa japo kuna mengine yamefanyiwa ukarabati. Naomba speed iongezeke ili kuweka mazingira mazuri ya watoto wetu kusoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, viongozi wa vyuo. Kumekuwa na uteuzi wa maprofesa wengi kumsaidia Rais kazi za siasa na kuacha ombwe kubwa katika sekta ya elimu. Tunaomba kama hakuna haja wangeachwa waendelee na kazi ya kufundisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, siasa vyuoni. Kumekuwa na upendeleo kwa vijana wetu vyuoni kwa kuangalia vyama. Vyuo kama DUCE na Mwalimu Nyerere wanatoa kumbi zao kwa vijana wa CCM ili kufanya siasa wazi na kuleta mgawanyiko kwa vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, pads. Tunaomba punguzo la bei za taulo za kike na zitolewe kwa wanafunzi husika kwa kutenga fungu na kusaidia tozo ili zifike kwa walengwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto wa kike, hasa majumbani na wapatapo shida hawana pa kuwatunzia wakati usuluhisho unaendelea hivyo kupelekea kurudi katika majumba yao ambayo sio salama kwa wakati huo. Nashauri Serikali ijenge majengo salama kwa usalama wa waathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na upungufu wa wodi za wanawake, hasa katika Hospitali ya Makandana, Tukuyu. Tunaomba Wizara kwa kusaidiana na Halmashauri ya Rungwe kutatua tatizo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimba za utotoni. Tunaomba Wizara itoe tamko kwa mabinti wapatao mimba katika umri mdogo kurudi shule hasa walio chini ya miaka 15 kwani kutorudi shuleni kunapoteza haki yao ya kupata elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, dawa/chanjo ya mbwa. Kwa wagonjwa waliong’atwa na mbwa matibabu ni ghali sana. Tunaomba Wizara ipunguze kama sio kutoa bure chanjo hizo kwa waathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, vipodozi hatarishi. Wizara na wadau wa afya kwa pamoja wafuatilie madawa/vipodozi hatarishi vinavyoathiri afya za wanawake na watoto. Kumekuwa na madawa yasiyo rasmi katika maduka mengi na dawa kama za kuongeza makalio, matiti, uume na hata wanaojichubua, Wizara ya Afya, TFDA na TBS kwa umoja wasaidie jamii yetu kutopata matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, uhaba wa watumishi. Wizara ipeleke wataalam hasa wa magonjwa ya wanawake na watoto katika Mkoa wa Mbeya, Wilaya za Chunya na Mbarali, ndiyo zenye changamoto kubwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kuhusu mipaka, Jeshi limekuwa linapiga na kuvunja na kubomoa nyumba za wananchi, kuchukua sheria mkononi kwa Jeshi siyo kitu sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fidia za wananchi kwa maeneo yao ina suasua kabisa na ikibidi kama ikishindikana warudishiwe maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu viwanda Jeshini, kuingia uchumi wa viwanda ni vyema tukawekeza katika viwanda vilivyoanza vya Jeshini kwani ni nguvu kazi iliyo tayari na ya uhakika lakini ukosefu wa fedha na kuwarudisha nyuma vifaa chakavu vinakwamisha ufanisi wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ulinzi wa mipaka, Jeshi lipatiwe vifaa na pesa zaidi ili kuhakikisha mipaka yetu inakuwa salama kama uwepo wa boti za doria na helkopta za ulinzi, ujenzi wa madaraja ya kupitisha vifaa vizito nyakati za dharura ni muhimu sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwamba nimepata nafasi ya kuchangia kama Mbunge kwa kuwa maoni yetu kama Kambi Rasmi ya Upinzani yameshindikana, tutayatumia kwa kuongea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Ndani - Fungu 28 tunalolizungumza leo ikiwepo Polisi na wenzao kuna upungufu mwingi sana unaotokea katika Wizara hii. Nikianza kwanza na suala la wakimbizi. Kuna sare za kijeshi zilikamatwa kwenye mipaka, zile sare zilienda zikachomwa, nakubali, lakini najiuliza wafanyakazi wetu wa Uhamiaji waliachaje zile sare zikaingia katika nchi yetu. Nataka kujua, mambo yapo mawili; kama Taifa la Tanzania tulikuwa na utaratibu wa kutoa taarifa tunapokuwa na watu wasiofaa katika jamii inayotuzunguka na kama kuna kitu kibaya kinatokea, sisi kama Watanzania na Jeshi la Polisi likiwemo na Immigration walikuwa wanapewa taarifa na wananchi, je, mahusiano yetu kama Jeshi la Uhamiaji yapo sawasawa na wananchi, ilikuwaje hizo sare zikapita?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye Jeshi la Polisi. Jeshi la Polisi imekuwa ni chama kingine cha siasa, kimejificha nyuma ya Chama Tawala Chama cha Mapinduzi. Sisi kama chama kilichosajiliwa CHADEMA na wenzetu wa CUF, ACT na vyama vingine tunahitaji kufanya siasa kwa ajili ya kuongeza wanachama na ni wajibu wa kikanuni na Kikatiba kwa sisi kufanya kazi ya siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wana neno wanatumia intelijensia. Intelijensia ipo kwa Wapinzani na wala sio kwa Chama Tawala. Nataka niwakumbushe Jeshi la Polisi, Tanzania hii amani iliyopo sio kwa sababu tuna jeshi kubwa, sio kwa sababu tuna siasa nyingi, lakini kwa sababu watu wote tumeamua kuipenda nchi yetu na tumeamua kukataza watu wetu watulie na siku ikibidi polisi hawawezi kutushinda kwa maana Watanzania pia ni wengi kama vile Polisi wanafikiri wao wanatuweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafanya mkutano Area A, Area D CCM inafanya mkutano, unakujaje kwenye ofisi yangu kwenye mkutano wa ndani umeshika tear gas kuja kunizuia na CCM hujawazuia? Polisi tunawaonya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua mnatumika kwenye chaguzi kuja kubandika matokeo ambayo siyo kazi yenu. Mheshimiwa Siro nakuheshimu, naomba simamia taaluma ili uweze kuwazuia askari wako kwa sababu mwisho wa siku hawa ni ndugu zetu, tunaishi nao uswahilini, tunasoma nao na tunakwenda nao sokoni. Naomba tusifike tukagombana kwa sababu ya siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi linazuia Wabunge wenye majimbo kufanya siasa. Mheshimiwa Kubenea wiki mbili zilizopita kazuiwa kwa kitu kinaitwa intelijensiia lakini Mheshimiwa Mchengerwa anafanya mkutano intelijensia haipo. Nchi yetu ni ya umoja, tumeishi kama ndugu, msitutenge. Kama mnataka siasa vueni vyeo ingieni kwenye siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vitambulisho vya Taifa. Walioandikishwa ni 19,000 mpaka sasa ni milioni nne tu ndiyo wamepata vitambulisho hivyo na hawa watu wameshindwa kwa sababu hawana pesa, wanadaiwa na mkandarasi. Serikali haijatoa hela, uzalishaji wa vitambulisho ni kidogo, leo hii mnalazimisha matumizi ya Kitambulisho cha Taifa wakati wajibu wa Serikali kutoa pesa hamfanyi. Serikali yako iseme hapa tarehe hiyo 1 Mei waliyoweka ya matumizi ya kitambulisho wazuie mpaka haki ya Watanzania ya kupata vitambulisho ipatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni iliyochukua tenda ya kutengeneza mashine za hivyo vitambuliso kutoka Malaysia wameleta mashine ambayo uzalishaji wake ni mdogo na mpaka leo kuna watu waliwekwa ndani, sina uhakika kesi zinakwendaje. Mheshimiwa Waziri akija kujibu atuambie hatua zilizochukuliwa, pesa za Watanzania zilizopotea na wale waliosababisha ufanisi mbovu wamechukuliwa hatua gani mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi tena kwenye Polisi maana yake hawa ndiyo cancer ya Taifa. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua ni kanuni ipi na ni njia gani inayotumika Polisi ambao wanajua kazi yao ni kulinda mali za Watanzania lakini Polisi hao hao wanakwenda kuwagawa Watanzania kwa itikadi za kisiasa. Ma-OCD, ma-RPC, wote wanasimamia kazi za kiasiasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Wabunge wote wa Upinzani wakitembelea majimbo yao OCD yuko mgongoni. Tunakubali, tunahitaji ulinzi, tunafanya kazi kwa sheria na sisi tumejipanga kuwa waaminifu lakini wanatuchokoza na muda mwingi sana tumewavumilia. Tunafanya mikutano wanashinda na kamera kuturekodi, mikutano ya CCM mbona hawarekodi? Tunawatangazia Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Vitongoji na Uchaguzi Mkuu, tunajua kuna maelezo toka juu kama yapo na sisi tutayafanyia kazi maelezo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa siku Jeshi la Polisi litueleze shilingi bilioni 16 za sare za Polisi ambapo pesa zilitolewa na mwisho wa siku kuna uniform hewa, ziko wapi? Hii ni kwa mujibu wa CAG.

Naomba kujua matumizi ya fedha hizo na ambazo walipata kutoka kwa wahisani ili kujenga vituo vya mifano ambapo Polisi imeshindwa kufanya. Tunaoma watuambie na hasa Mheshimiwa Kangi Lugola, uje utupe majibu sio ya kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kangi Lugola ni Mbunge mwenzetu lakini toka ameingia Jeshi la Polisi amekuwa na matamko zaidi ya 20 hata moja hakuna lililotekelezeka. Kuna wakati anatoa matamko kumbe amekosea, sijamuona akirudi hadharani na kuomba msamaha. (Makofi)

MHE. JUMA S. NKAMIA: Kangi hajaingia Jeshi la Polisi, ameingiaje Jeshi la Polisi?

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kangi mara nyingi ameonekana akishusha watu vyeo labda huyo mtu kakosea lakini si haki kwa Jeshi la Polisi kumdhalilisha hadharani, kuna njia sahihi za kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiongelea habari ya Magereza, Magereza kuna msongamano mkubwa na kibaya zaidi magereza ya wanawake wafungwa maeneo ya kuwahifadhi na kujihifadhi nayo ni madogo na wanapata shida sana. Tunaomba Magereza watazamwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jengo la Mchicha kwa Zimamoto, nimelizungumzia mara nyingi. Ni kitu kibaya kutumia pesa za Watanzania tukazi-dump pale Mchicha halafu tunashindwa kufanya mipango ya miaka mingi, tunatumia akili zetu nyingi kuzuia Upinzani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongelea suala la uniform za wafungwa. Uniform ni haki kwa mfungwa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Mpango huu wa Maendeleo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2018, nilisimama hapa na nikaongea na Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango kumwambia kwamba mipango tunayoipanga kama Taifa na Bunge likaridhia na tukapitisha, ni vyema Serikali ikasikia yale ambayo tumeyashauri na kuyatendea kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ina zaidi ya asilimia 70 ya wananchi ambao ni wakulima. Cha kushangaza, bajeti iliyopita tulipata shilingi bilioni 100 iende kwenye kilimo ili iweze kusaidia shughuli mbalimbali ikiwemo utafiti, shughuli za kilimo na mambo mbalimbali ya Wizara husika. Napenda kusikitika kwamba imetoka shilingi bilioni mbili peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia kilimo ni uti wa mgongo, kwa sababu najua kauli hii haijatenguliwa toka tumepata uhuru wa Taifa hili; leo hii ambapo wakulima ni wengi huko vijijini na hususan wanawake tunaowawakilisha, kama hujapeleka pesa unakuwa hujawatendea haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili ufanikiwe katika viwanda, tunasema kwamba sasa hivi tunaenda kwenye viwanda vya kati kama Taifa. Usipowekeza kwenye kilimo, ambapo kilimo ndiyo kinatoa malighafi kwa viwanda hivi, unakuwa bado unafanya siasa kwenye mambo ya makini ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika asilimia 100 ya bajeti ambayo Bunge lako Tukufu lilipitisha, asilimia 98 ya gawio la fedha Mheshimiwa Dkt. Mpango haikupelekwa. Ninaomba tunapopanga vitu na Bunge lako likaridhia, Serikali na Wizara iweze kuachia fedha kwa ajili ya watu hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maafisa Ugani ni wachache. Kwa mfano, nikichukua tu kwenye Wilaya ya Rungwe, wasimamizi wa kilimo wako wachache, hawawezi kufikia wakulima wote. Tuna Chuo cha Uyole Mbeya; Chuo kile kinasaidia utafiti. Huwezi kuwa na kilimo kisichokuwa na Utafiti. Tunataka kujua ni ng’ombe gani bora wenye mbegu bora kwa ajili ya kilimo? Utawezaje kujua pasipo utafiti?

Mheshimiwa Mwenyekiti, chuo kile takribani miaka mitatu sasa hakijapelekewa fedha za maendeleo, unawezaje kuwasaidia wasomi hawa ambao wanasimamia raslimali za Taifa na ni washauri wa kundi kubwa la wakulima? Hawana fedha. Naomba Wizara yako Mheshimiwa Dkt. Mpango iliangalie suala hili kwa umakini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia pembejeo. Tumekuwa na kilio kikubwa sana juu ya pembejeo. Leo hii kuna mbegu za aina mbalimbali na nyingine hazioti, wakulima wanalalamika. Tumesema Maafisa Ugani ambao wangetusaidia, leo hii ajira ya kuwaleta na kutuongozea kule vijijini hawapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tujipange na bahati mbaya sana tumebaki na mwaka mmoja kama siyo miezi sita ili tuweze kumaliza mipango tuliyokuwa tumejiwekea. Naomba tafadhali tusimame kwa yale tunayoyasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunapozungumzia mbolea, kuna sehemu nyingi sana; sehemu za Mbarali na sehemu nyingine mbalimbali ambazo mimi nawakilisha, mbolea inaenda kwa kuchelewa. Wakati mwingine Mawakala mnaowapa wamekuwa hawawatendei haki wakulima jinsi ambavyo ilipaswa wafanye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niache hapo, niende kwenye suala la elimu. Taifa lolote likitaka kukandamiza watu wake linaweka elimu kuwa ni ya hali ya chini. Usipowekeza kwenye elimu, umeandaa jeshi la watu wajinga ambao watakuwa rahisi sana kupotea. Elimu kwa bajeti ya maendeleo iliyopita tuliweka shilingi bilioni 249. Sasa mnasema elimu bure, elimu isiyokuwa na malipo. Ni kweli ukitamka shilingi bilioni 200 kwa mwananchi wa kawaida anaona ni fedha nyingi, lakini ukienda kwa Mwalimu wa Shule ya Sekondari kwa mfano, anakwambia amepewa shilingi 200,000/= Capitation. Shilingi 200,000/= anunue chaki, alipe mlinzi na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri tunahitaji kuwekeza zaidi. Tunaposema bure, nafikiri bora turudishe kama tulivyokuwa mwanzo, kwa sababu wananchi walijitolea wakatusaidia, watoto wote walikula chakula cha mchana. Ukisema bure, kuna wazazi wengine wamegomba kutoa michango kwa sababu Serikali imesema elimu ni bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni nyumba za walimu. Hiki ni kilio kikubwa sana. Walimu wengi wamepanga, wanakaa mbali na maeneo ya shule. Mishahara haijaongezeka. Mheshimiwa Waziri, hebu tuwatazame walimu, maabara na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matundu ya vyoo ni tatizo hususani kwa watoto wa kike. Nazungumzia suala la bajeti. Tunapopitisha pesa, mashirika mengi, Wizara nyingi zinapata robo ya mapato inayostahili kupata. Sasa inakuwa kama vile; aidha mtuambie Serikali haina hela, lakini Serikali ya Awamu ya Tano inasema ina hela nyingi. Sasa bajeti ya shilingi bilioni 100, unapata shilingi bilioni mbili. Tunaomba maelekezo ya kina, kwa nini Bunge linapitisha halafu fedha inayotoka inakuwa kidogo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni deni la Taifa. Mwaka 2018 nilizungumza juu ya deni la Taifa. Tumevuka sasa zaidi ya shilingi trilioni 50. Naomba, na nilisema mwaka 2018 pia, tusikope pesa. Tulete sheria humu Bungeni Serikali isikope mpaka Bunge liwe limeridhia. Hii tabia ya kukopa pesa hatujui tunalipaje, deni la Taifa limekuwa kubwa na mnasema ni deni himilivu na mna lugha zetu za kisomi, lakini mwisho wa siku wanaolipa madeni haya ni watoto ambao leo hawajazaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua Mheshimiwa Dkt. Mpango ni msomi, naomba asimamie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni mifugo na uvuvi ambayo ndiyo imeajiri sekta ya watu wengi. Kwenye uvuvi tulitoa shilingi bilioni nne ya maendeleo, tunarudi pale pale kwamba ni asilimia tatu ya fedha ndiyo iliyotoka. Tuna maziwa makubwa; Ziwa Nyasa, Ziwa Victori na Ziwa Tanganyika, kama Taifa tusipojipanga juu ya kutumia maziwa haya kuleta maendeleo kwa vijana wetu, nafikiri tutakuwa tunajidanganya. Unafanyaje maendeleo pasipo kuwawezesha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna maendeleo bila demokrasia. Ndugu zangu wameongea habari ya demokrasia. Leo hii tunapanga mipango lakini kwa njia ya figisu mmewaengua watendaji ambao ndio waleta maendeleo. Mnaendeleaje? Tukae chini kama Taifa, tuache uwoga, tufaanye kazi kama team. Leo hii mmeumiza watu wengi nafsi zao na kujiandikisha wameona ni kitu cha kupoteza muda. Tunaomba demokrasia ichukue nafasi yake. Wengine wameumizwa na wengine wako ndani. Hivi ni watu gani wajinga wasioona? Kwa sababu mwisho wa siku, watu wanaishi na watu kule chini. Mmetupa watu ambao sisi hatujawachagua, tunapangaje maendeleo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, demokrasia ni tunda la haki. Pasipo haki, amani haiwepo. Naomba tusimame na hilo, tuwasimamie Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono Kambi Rasmi ya Upinzani. Ahsante. (Makofi)
Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba Kigosi Kuwa Hifadhi ya Taifa Kigosi pamoja na Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji wa Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba la Igalla Kuwa Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu Zebaki (Minamata Convention on Mercury)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mimi niweze kuchangia hoja iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi hakuna mtu anayeweza kupinga maendeleo ya Kitaifa ikiwepo kutunza hifadhi zetu na kuweza kutambua maeneo mbalimbali yakafanyika kuwa hifadhi, mimi mwenyewe mmoja wapo ninapongeza Wizara ikiendelea kufanya hivyo, lakini ikifuata kanuni na sheria za Kikatiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mzungumzaji aliyepita ametoka kuzungumza mahali hapa kwamba watu wa lile Pori la Ugalla walikuwepo siku zote na Serikali hii ilikuwepo, wananchi wale wakapewa huduma mbalimbali, huduma za umeme, maji wameendelea kuishi kwa miaka na kufanya mifugo yao mahali pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachotaka Serikali itoe taarifa kwa wananchi, wakaweza kutoa na elimu na kuwaelimisha wananchi ili waweze kujua maendeleo yao, maana yake mwisho wa siku walinzi wa hifadhi wa hizi ni hao hao wananchi wanaoishi maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania hawa wamezaliwa katika maeneo hayo, leo hii tukiwafanya wakimbizi katika nchi yao tunakuwa hatuwatendei haki. Mpaka sasa Serikali inaleta hoja hii mezani kwako hata Kamati yenyewe haijafika kwenda kukagua maeneo husika na kuona ni jinsi gani wananchi wameathirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumza wenzangu juu ya TANAPA, TANAPA tumeipatia mzigo mkubwa na ndiyo kazi yetu offcourse lakini je, bajeti tunazopanga kwa Mheshimiwa kiongozi huyu wa TANAPA, je, pesa hizi zinamfikia ili aweze kufanya kazi yake kwa ufanisi na kazi akafanya kwa uweledi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vibaya zaidi kuongeza kazi zaidi wakati pesa Serikali haitoi kwa TANAPA wala haitoi msaada wa kuisaidia TANAPA kuweza kufanya kazi yake vizuri, hata tunapoingia kwenye ushindani wa utalii ni lazima mapori haya yawekwe kimpango mzuri hata kuweza kuvutia hawa watalii, lakini kama hawana pesa wanajipangaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya wananchi katika hizi hifadhi zimekuwa za muda mrefu, tunaomba Wizara hata kama leo mnapitisha kwa kura nyingi...

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA:...mbazo ziko upande wa pili, tunaomba Mheshimiwa Waziri Kigwangalla uende ukahakikishe hiyo migogoro kwa ukaribu sasa, japokuwa tumetangulia mbele wewe utakuwa unarudi nyuma, wananchi wakaweze kutatuliwa matatizo ya kwao, tunakuomba ufanyie hivyo bwana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Waziri tunataka tujue katika vijiji kwa mfano kwa upande wa hili Pori la Ugalla kuna watu wa Sikonge na Kaliua mmekataje? Ni kiasi gani ambacho kitaenda kwenye hifadhi mtuambie na kiasi gani ambacho kitabaki kwa wananchi, kilio changu mimi bado ni wananchi, kwa sababu tunajua mwisho wa siku wananchi hawa mmeshawawekea mawe, kuna wakati Mbunge wa Kaliua aliwahi kuzungumza hapa kwamba mnaweka mawe mpaka kwenye vitanda vya wananchi.

Sasa tunaomba Mheshimiwa Waziri kama Mtanzania, naomba urudi tena ukaangalie uhalisia wa Mheshimiwa Mbunge aliyezungmza katika Bunge hili, kama ni kweli vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya ninaunga maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza kabla sijaongea ninapenda kutoa pole kwa Kiti cha Spika pamoja na wewe pamoja na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi walioondokewa na kiongozi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nitumie nafasi hii kumpongeza Rais wa kwanza mwanamke, mama Samia Suluhu Hassan akituwakilisha wanawake ambao tunaona maono mbele ya kutetea Taifa hili la Tanzania na kwenda mbele kupambania haki za wanawake, wanaume na watoto wa nchi hii; ninampa pongezi. Yeye alipoapishwa tarehe 19 aliongea maneno ya matumaini kwa Watanzania; alisema tuache yaliyopita sasa tuijenge Tanzania mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nimuombe mama Samia Suluhu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nchi yetu ni moja na sisi sote tumezaliwa Tanzania kwa kusudi la Mungu. Tunamuomba asimame kama Rais wa watu wote, Rais wa vyama vyote. Ninamuomba Mheshimiwa Rais pamoja na pongezi tunazompatia, tunaomba agange majeraha yaliyowapata Watanzania hasa wakati wa uchaguzi. Aweze kuwaachilia wafungwa wa kisiasa ambao bado wapo magerezani, hasa wale waliokuwa wamesingiziwa. Waliokosea, sheria ichukue mkondo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Rais tunayempongeza leo alikuwa Mwenyekiti wa Bunge la Katiba. Tunaomba sana Mheshimiwa Rais uanzie pale ulipoishia, Katiba ya Warioba tunaomba uanzie hapo kulisogeza mbele Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua kwamba tangu ameapa kuwa Rais nchi imetulia, imeanza kupoa, watu wameanza kupata amani. Tunaomba amani hiyo yeye kama mama aisimamie, ahakikishe anasimama kama Amiri Jeshi Mkuu anayetetea pande zote bila kubagua. Tumeona viongozi baadhi ya vyama wameanza kuomba msamaha; hiyo ni dalili njema ya kujua kwamba kiongozi aliyepo sasa anasimamia haki, atasimamia Katiba na ataijenga na kuisimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, ninasisitiza tena; ninakupa pongezi Mheshimiwa Rais, kwamba utasimamia haki na Katiba ya Watanzania kuhakikisha tunakwenda mbele maana safari bado ni ndefu, Tanzania bado ni imara, wewe ndiwe tunakutegeme kuijenga na kuisogeza mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya nasema ahsante sana. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi na mimi nichangie hotuba ya Rais. Kabla sijaendelea naomba nimshukuru Mungu kwamba amenipa maisha na amenisaidia kuwa mzima mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeangalia katika hotuba ya Rais ukurasa wa 10, alijikita kuzungumzia mambo ya viwanda. Viwanda ndivyo vinavyotoa ajira kwa vijana na ndivyo vinavyoongeza pato kwa Taifa. Ni kweli kwamba kuna kipindi tulibinafsisha viwanda na kwenye ukurasa huo Mheshimiwa Rais alizungumzia kusuasua kwa viwanda vilivyobinafsishwa.

Mheshimiwa Spika, viwanda vingi vilinunuliwa na watu wakabadilisha matumizi, siyo kama vile kusudio lilivyokuwa. Sisi katika Mkoa wetu wa Mbeya, Kiwanda cha Zana za Kilimo (ZZK) leo hii ukienda unakuta mtu amekodisha ghala za kuhifadhia pombe kwa ajili ya kuuza kwa bei ya jumla. Nafikiri ni wakati sasa Serikali ifuatilie kwa wale watu ambao walibinafsishwa na wakasema wataendeleza kile kilichokuwa kikiendelea wakabadilisha matumizi, ninaomba Serikali isimamie hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika viwanda watu wengi wanataka kuwekeza, lakini unapotaka kuanzisha viwanda, kodi zinakuwa nyingi, lakini pia ufuatiliaji wa kodi hizo, unaenda madirisha mengi; unaenda TRA, unaenda sijui kwa watu wa viwango na vitu kama hivyo. Nashauri Serikali iweke dirisha moja ili watu waende kwa wakati mmoja, wafanye vitu vyote mahali pamoja.

Mheshimiwa Spika, viwanda vingi sana hapa nchini vingeendelezwa vingeweza kusaidia ajira ya vijana. Kwa mfano, hapa Tanzania tuna zao la ngozi. Kwa bajeti ya mwaka jana wauzaji wa ngozi nje ya nchi wamepoteza takribani milioni 200 kwa kukosesha kwenda kuuza ngozi kwa sababu ziliharibika. Ninaomba urasimu katika kusaidia wafanyabiashara ya ngozi nje ya nchi, upunguzwe ili tuweze kuona vijana wetu wakipata ajira katika viwanda hivi. Maana ni zaidi ya vijana 400 ambao walikosa ajira mwaka 2020 baada ya ngozi hizi kushindwa kusafirishwa.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Rungwe kuna Kiwira Coal Mining ambayo ilibinafsishwa. Iliajiri wanawake wengi na vijana wengi, lakini mpaka leo imekuwa gofu. Hata hilo wazo la kwanza la Baba wa Taifa kuona inafaa kwa Taifa letu la Tanzania, ndoto za Wanakiwira pamoja na Wanambeya zimeishia hapo baada ya kufunga migodi kama ile.

Mheshimiwa Spika, nasema viwanda bila kilimo haiwezekani. Watu zaidi ya asilimia 75 ni wakulima. Ili uweze kupata malighafi ni lazima uwekeze kwenye kilimo. Leo hii tunalalamika habari ya pembejeo. Mheshimiwa mmoja amesema hapa, tunategemea mvua. Ni wakati sasa wa kubadilisha kilimo chetu, ni wakati wa kuona kilimo ni uti wa mgongo kama mbiu ya zamani ilivyokuwa inasema. Tuanzishe umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, bajeti ya mwaka 2019/2020 tulipitisha hapa Bungeni takribani shilingi bilioni 37 kwa ajili ya umwagiliaji. Hata hivyo, ni shilingi bilioni nne tu zilitoka kwenye Wizara ya Kilimo. Ninashauri, Bunge linapopitisha bajeti, ni vyema Serikali ikajikita kusaidia ili iweze kupeleka maendeleo kwa watu wetu na hasa wakulima.

Mheshimiwa Spika, kilimo bila utafiti haiwezekani. Ili uwe na kilimo bora, lazima uwekeze kwenye asasi au taasisi za utafiti. Tuna Uyole pale Mbeya, ni Kituo cha Utafiti. Huu ni mwaka wa tatu sasa hawajapata fedha kwa ajili ya utafiti. Pana mitamba pale, ili uweze kujua mbegu bora ni lazima wasomi wetu SUA na sehemu nyingine wafanye utafiti. Naiomba Serikali iwekeze kwenye utafiti ili tuweze kupata mbegu bora.

Mheshimiwa Spika, TARURA, watu wengi wamezungumzia habari ya TARURA, zamani ilikuwa kwenye Halmashauri. Labda kwa kusema leo, jana nilimsikia Mheshimiwa Jafo akizungumza, vitu vingi vimerudi kwenye Halmashauri.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi nami niweze kuchangia mada iliyokuwa mbele yetu. Naomba niwakumbushe waumini wa makanisa 142 ya Gwajima, lakini pia waumini wa Tanzania juu ya Biblia inasema nini? Biblia inasema, katika Marko 16:18a, “hata tukila vitu vya kufisha, havitatudhuru.” Hivyo basi, napenda kumwambia Askofu Gwajima kwamba, Biblia hiyo inazungumzia hata nikichanja chanjo iliyokuwa na sumu kama, imani yake yeye kama Askofu, hafahamu kwamba chochote kibaya kitakachoingia kwa waumini wake hakina madhara katika miili yao sawa sawa na Biblia inavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Biblia hiyo hiyo inasema katika Waefeso 6:12 inasema hivi, “kwa maana kwetu sisi damu na nyama, bali si juu ya wafalme na mamlaka ya nguvu za giza, vita vyetu sisi ni vya katika Ulimwengu wa Roho.” Sasa kama yeye ni mtu wa imani, kama tukibebwa katika imani kitu chochote kibaya hakitawapata Watanzania na ndivyo tulivyo na ndiyo maana tunaenda mahospitalini tunatibiwa, Wakristo wanajenga zahanati, wanajenga hospitali, kwa sababu tiba ni sehemu ya mamlaka ya Mungu. Hata Nabii Luka aliandika Kitabu cha Luka alikuwa ni daktari maana Biblia inawatambua madaktari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Biblia hiyo hiyo inasema, katika Waebrania 11:1 “imani ni kuwa na hakika na mambo yatararijiwao ni bayana na mambo yasiyoonekana.” Ukiwa na imani hakuna kitu kibaya kitakupata. Gwajima usiwakwamishe Wakristo wako na Wakristo wa Makanisa 142, imani itatulinda kama Watanzania, tutakula dawa na vitu vibaya havitatupata maana tunamwamini Mungu, na Mungu yupo katika Taifa la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waraka wa Tatu wa Yohana 1:2 inasema: “Mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yako yote, katika mambo yako ya rohoni na ya mwilini.” Hivyo basi, Biblia inatamka mwananchi wa kawaida afanikiwe mwilini, afanikiwe katika roho. Kuchoma sindano ni haki na ndiyo maana hata Gwajima akiumwa anakunywa panadol kwa kuwa Serikali inaamini Biblia inatambua katika matibabu.

Mheshimiwa Spika, walikuwepo viongozi wa dini ambao mapepo yaliwavaa; amemsema ndugu Kibwetere. Katika mwaka 2000 Machi, 17 alichoma kanisa na watu walikufa. Naomba tusimame katika imani ya Mungu, tusiwadanganye wananchi. Nanyi wananchi someni Biblia mjiamini. Ndiyo maana ukienda kujifungua, kama wewe ni Mkristo unakwenda hospitali kwa nini? Kwa sababu madaktari wana elimu ya kimungu. Hujifungulii nyumbani. Gwajima asiwadanganye watu. Ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nami kupata nafasi ya kuchangia Mpango huu wa Tatu tunaouendea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mpango unaandaliwa kulikuwa kuna malengo hasa waliyafikia. Kwanza kulikuwa na mambo kama manne kwa sababu ya muda nitayataja, viwango vya juu vya maendeleo ya viwanda lakini pia ushindani, maisha bora na utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili uweze kutimiza haya malengo kulikuwa kuna viashiria, kwa mfano, walisema kuwekeza kimkakati katika viwanda vya nguo za pamba pamoja na mazao ya mbogamboga. Leo hii katika nchi hii ya Tanzania na hasa nikizungumzia Nyanda za Juu Kusini, wanalima mazao ya mboga mboga, wanalima mazao ya biashara lakini hatuna soko la uhakika. Ndugu zangu hapa wamezungumzia Maafisa Ugani. Leo hii ukienda Mkoa wa Mbeya, utakuta wakulima wanalima kutokana na wanavyosikia kwenye mikeka au kwenye vikao vya chini wanavyokaa na wala sio kwa utaalam. Leo wanakwambia zao la chai ni zao ambalo linauzika duniani na hatujawahi kusikia chai imeshuka katika soko la dunia, lakini hakuna Afisa Kilimo anayekwenda kuwasaidia wakulima wa chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo chai inauzwa Sh.200 kwa kilo wilaya ya Rungwe, lakini ukienda Njombe chai inauzwa Sh.500 kwa kilo. Ukienda Lushoto, chai ni Sh.500 kwa kilo. Ni nchi moja, Serikali moja, bei tofauti. Tumelilalamikia hilo na tunaendelea kuuliza kwa nini tuna Bodi ya Chai inayofanana bei zinaenda tofauti, uchumi unakua hauendi sawa, watu wa Mbeya wanapata kidogo, watu wa Lushoto wanapata zaidi. Tunaomba Serikali na hasa Wizara ya Kilimo isimamie suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii kuna mazao ya vanilla. Mkulima anaamua kulima vanilla kwa sababu jirani yake kalima vanilla. Anaambiwa kilo moja ni 400,000 sasa tunataka Maafisa Kilimo waende wawaambie wananchi kama ni kweli hiyo bei iko kwenye soko badala ya watu kuambiana na kuwa na vikundi vya kuambiana zao hili linalipa, lakini mwisho wa siku akilima vanilla kwa miaka miwili anakuta soko Sh.50,000 na ametumia gharama kubwa. Tunaomba Wizara ya Kilimo isimamie suala hilo lisaidie wananchi wasifanye kilimo cha makundi au kusikia kwenye redio mbao, ifuate mfumo wa Serikali kwa kupitia Maafisa wetu wa Kilimo kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia biashara ya ushindani, leo hii tuna Bandari ya Dar es Salaam, ni bandari ambayo Mungu ametupa wala hatujaitengeneza, ipo. Leo Bandari ya Dar es Salaam kama tusipofanya kwa umakini kama wananchi wa Tanzania Beira inachukua wateja wetu wote wanapeleka Bandari ya Beira, watapeleka Bandari ya Afrika Kusini. Hivyo tunaomba viongozi wetu ambao wamesomea mambo ya marketing wajitahidi kusimamia biashara yetu ili Bandari yetu ya Dar es Salaam iendelee kupata wateja na wateja wasitukimbie kwa sababu ya vile viwango vinavyowekwa. Mtu akienda Beira anapewa labda siku 21 ndipo anaanza kulipia mzigo wake. Ukija kwetu mnawapa siku 14. Ni lazima tuwe wajanja na kufikiria kwamba wanaotuzunguka Mombasa na wengine hawapendi maendeleo ya Tanzania, hivyo basi viongozi wajifikirie kujiongeza, wahakikishe wale wateja ambao walikuwa wanapitia bandari yetu, hatuwapotezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viwanda, huwezi kuzungumzia viwanda ukaacha kilimo. Leo hii tunahitaji kupata malighafi kutoka kwenye kilimo ili viwanda vyetu viweze kupata malighafi hapa hapa nchini. Naomba sana tuhakikishe kwamba kilimo hasa mbolea na pembejeo zinafika kwa wakati kwa wakulima. Nilizungumza hata hotuba iliyopita, bila utafiti hatuwezi kufanikiwa, tuwekeze kwenye utafiti. Nilisema last time kwamba tuna Chuo cha Uyole ambao wao ni wenzetu wamesomea mambo hayo, tuna SUA na asubuhi umezungumza hawa watu wa SUA wajikite kwenye utafiti ili kusaidia watu wetu na kilimo chetu tupate mazao ya kutosha ili yaweze kusaidia kwenye viwanda na tuweze kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utalii; leo hii tuna majirani zetu wa Kenya, sisi tuna vitu vingi sana vya utalii lakini kuvitangaza tumeweka bajeti ndogo sana. Leo hii mikoa mingi sana ina vivutio lakini Kaskazini ndiyo inaonekana ina vivutio vingi kwa sababu Serikali imewekeza huko zaidi. Kuna vivutio vingine ni vidogo. Ukienda sehemu za Njombe unakutana na bustani ya Mungu, unakutana na maua mazuri, tujitahidi kueleza watalii wetu kwamba hata huko pia wanaweza wakaja na uchumi ukaongezeka. Tuna daraja la Mungu sisi kwetu Rungwe, je, watu wetu wanafikaje? Ukienda kwenye daraja la Mungu miundombinu kufikia ni kilometa tano kutoka barabara kuu lakini mpaka ufike barabara ilijengwa na Mjerumani mpaka leo hakufikiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwango vya kutoza watalii. Nimerudia mwanzo nimesema viongozi wetu na wataalam waende hata kwa upelelezi wajue Kenya wanafanyaje na nchi zingine wanafanyaje na sisi tuone kama tunapunguza au tunaongeza kwa faida ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango ulisema uchumi utakua mpaka asilimia 10, ule ulikuwa ni Mpango, lakini mpaka sasa bado hatujafikia, tunahitaji kukaa na kujipima ni wapi tumekosea, ni wapi tuongeze nguvu ili tuweze kuhakikisha tunasonga mbele kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengi sana ambayo sisi kama Taifa tunafikiri tukisimamia tunaweza tukasonga mbele. Tunazungumzia maisha bora, ili Mtanzania wa kawaida asilalamike kusema mnasema uchumi umekua, mfuko wangu hauna pesa, ni lazima mzunguko wa fedha uachiliwe kwa wananchi. Unapomlipa mkandarasi kwa wakati, mamantilie atawauzia wale wafanyakazi kwenye barabara, mamantilie yeye akishauza chakula atalipa ada ya mtoto, pesa zitakuwa mfukoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kulipa madeni kwenye Halmashauri zetu, tunahitaji kuwekeza zaidi kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia utawala bora msipokuwa na amani, nakumbuka kuna Waziri mmoja alijibu hapa akasema utawala bora hapa pana amani. Sote tunafahamu unapozungumzia amani lazima uzungumzie na haki. Tulikuwa na uchaguzi uliopita, uchaguzi uligubikwa na mambo yasiyokwenda sawa kuanzia kwenye wakati wa kujiandikisha, wakati wa kutangazwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sophia, naona kengele kama vile.

Unasikia, imeshaita tayari. (Kicheko)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kuweza kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa ninapenda kuikumbusha Wizara hii mwaka 2017, 2018, 2020 kuja 2021 tulizungumzia suala la bima ya afya kwa wote. Taifa lisilokuwa na watu wenye afya haliwezi kuingia kwenye uchumi wa kati. Taifa ambalo lina wazee wengi waliolitumikia lakini hawana bima ya afya kuwasaidia hatuwezi kuwatendea haki wazee hao waliotumikia Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, lakini taifa lenye watoto wenye siku moja na miaka mpaka mitano wasiokuwa na bima tunawaweka katika matatizo makubwa sana ya kiafya na hatima yake hatuwezi kupata Watanzania ambao watatumia akili zao kwa sababu afya zao zina mgogoro na hawana bima ya afya.

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Wizara, kwa sababu Wizara ya Afya ilizungumza kwenye bajeti ya 2017/2018, kwamba wataleta bima ya afya, na wewe ulisisitiza sana; tunaomba tafadhali sana tulete kwa hati ya dharula tuweze kupata bima ya afya kwa wote, maana bila afya kuna mgogoro.

Mheshimiwa Spika, kuna magonjwa ambayo hayaambukizi. Leo hii tuna watu wengi wenye magonjwa ya kisukari, tuna watu wenye magonjwa ya figo, gharama zake ni kubwa sana. Tunaomba Watanzania hawa wawekewe bima ya afya maana ni haki yao ya kimsingi kuhakikisha afya zao ziko salama.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la kilimo. Asilimia themanini ya watu na wananchi wa Tanzania ni wakulima, na kilimo ni uti wa mgongo. Ninafahamu na ninamkumbuka Baba wa Taifa kwa kauli mbiu hii kwa Watanzania wote. Leo hii tunapozungumzia kilimo tunategemea kilimo kinachotegemea mvua pekee. Ninaomba, sasa tuna miaka 60 ya uhuru, tunahitaji kuhakikisha kilimo chetu kinakuwa sio kilimo cha chakula pekee kwa maana kwenda mdomoni, tunakataka kilimo cha Biashara.

Mheshimiwa Spika, ninafahamu tuna ekari nyingi sana hapa Tanzania na Watanzania wengi ni wakulima wanaotumia zana za kizamani. Na wale wawekezaji wanaokuja asilimia kubwa wao wanapewa ardhi iliyobora na wao wana mitaji mikubwa kwa sababu walikotoka wanakopeshwa. Watanzania hawakopesheki kwa sababu hawana vitu vya kuweka kama rehani kule benki na hivyo wanabaki kuwa wakulima wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wangu wa Mbeya tunafahamu Mikoa mitano ya Mbeya, Ruvuma tukienda na Iringa zile big five ambazo zilikuwa zinasaidia Taifa hili na kulisha nchi nzima leo hii Benki ya Kilimo inayokopesha wakulima ipo Dar es Salaam na wala haipo Mbeya, wala haipo Ruvuma, wala haipo Iringa. Tunaomba tuifanye benki, hii ni benki ya wakulima…

MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA:… wakulima wetu wanalima, leo hii tunalima parachichi, Wakenya wanakuja kununua parachichi…. (Makofi)

MHE. ALLY A. J. M. JUMBE Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Pokea taarifa Mheshimiwa Kagenda

T A A R I F A

MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa msemaji kwamba Benki ya Kilimo ipo Mkoani Mbeya pale mjini karibu na Bojan na imetenga mwaka huu bilioni 17.8 kwa ajili ya Mkoa wa Mbeya. Ahsante. (Makofi)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika

SPIKA: Mheshimiwa Mwakagenda, pokea taarifa, kumbe huna habari

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ninayo habari, hujo ndiye kaka yangu, Amenye, naomba niendelee.

Mheshimiwa Spika, leo hii mkulima anayelima mchele pale Kyela ambako ni kakangu sasa hivi ametoka kusema, anashindwa kupata mbolea kwa wakati, anashindwa kupata mbolea kipindi cha upandaji wa Mpunga. Anasema habari ya benki kule kwao Mwaya ndugu zake walioko Mwaya hawana hata fedha ya kukopa kwenda kulima mpunga maana kumbuka mpunga wa Kyela ni mpunga bora Afrika hata Nyerere alikuwa anatoa gunia moja la mpunga kwa Wajapan wanatupa gunia kumi leo hii wanakyela hawana hela ya kukopa kwa ajili ya mashamba ya mpunga.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia kilimo tunazungumzia pia masoko. Tunalima leo maparachichi ni kweli tunauza sasa hivi Shilingi 1,400 kwa kilo, lakini soko la dunia parachichi moja wanasogeza bei inauzwa kwa bei at least dola moja. Kwa nini Wizara hii ya Kilimo, ndugu yangu Bashe ninaomba utusaidie, kwamba mkulima kutoka shambani asiwepo dalali wa katikati apeleke moja kwa moja Australia akauze na mchumi wa Mtanzania ukapanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia masoko, nazungumzia soko la chai, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja Wilayani Rungwe; namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu aliona chai ya Rungwe inauzwa kwa bei ya kuonewa, kwa maana ya kilo Shilingi mia mbili wakati wenzetu wa Njombe wanauza kilo Shilingi mia tano. Mheshimiwa Waziri Mkuu ulifanya kituo chema, unafahamu, ukaweka tume ya kuchunguza kwa nini chai hii inauzwa kwa bei hiyo. Ninaomba Mheshimiwa Waziri Mkuu ukija utupe majibu sisi wana Rungwe na Wanambeya ile tume iliishia wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunazungumzia mifugo, mifugo pamoja na mazao yake, nazungumizia suala la maziwa. Leo hii kule kwetu Mbeya lita moja ya maziwa ni Shilingi mia sita, lakini utashangaa sana maji lita moja ni Shilingi elfu moja, mwekezaji wa maji anapata chanzo cha maji anaweka chupa ya plastiki anauza maji kwa Shilingi elfu moja kwa lita moja. Mkulima wa Mkoa wa Mbeya anauza maziwa kwa Shilingi mia sita yeye mkulima ni mtumwa wa ng’ombe, amkatie majani, ahakikishe anamtunza na madawa yake lita moja Shilingi mia sita. Tunaomba Serikali mtusaidie maziwa angalau yapande bei hata lita moja iwe Shilingi elfu moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Ngozi. Leo hii watanzania tuna ng’ombe nyingi lakini ngozi imewekwa zile alama sijui zinaitwaje, zinaondoa ubora wa Ngozi. Ninaomba ng’ombe wetu watafutiwe namna nyingine ya kuwatambua ile hali ya kuwachoma ng’ombe maalama tuipunguze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee habari ya miundombinu. Mimi nipo kamati ya miundombinu kwa mara ya kwanza nimeona SGR ikiwa imejengwa vizuri, tatizo letu sisi tulikuwa tunalalamika juu ya madeni ya taifa linapokuwa kubwa hatuoni kazi ikifanyika. Safari hii SGR tumekopa na fedha za ndani lakini kazi tumeiona.

Mheshimiwa Spika, pamoja na makofi haya ya furaha tunahitaji kuwajengea uwezo Watanzania kuweza kuitumia reli hii itakapokuwa tayari ili kukuza uchumi wa Watanzania. Ninaomba maeneo yale ambayo reli inapita tuhakikishe tumewawezesha Watanzania wale kujua umuhimu. Si tu hivyo ninaamini reli hii itasaidia yale malori yanayopita kwa wingi hasa njia yetu ya Dar es Salaam, Mbeya, Tunduma ambayo baada ya muda mfupi inaharibika ninaamini sasa watumie reli hiyo iliyotengenezwa ikiwepo SGR lakini na reli ya TAZARA bila kuisahau. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ninaamini sana kwamba kila kitu kikifanywa kwa makusudi au kwa bahati mbaya tunaomba sana sana utunzaji wa miundombinu hii, tuisimamie kama Taifa kwa umoja wetu. Ninampongeza sana Rais, Rais juzi ameenda kusaini mkataba ule wa Hoima. Tulipitisha sheria kwenye Bunge hili kwamba mkataba wowote ukipitishwa basi uje hapa Bungeni. Mimi ninampongeza sana kwamba at least tumemuona ameenda kusaini na sasa tunasubiri atuletee hapa Bungeni na sisi tujue ni kitu gani kizuri hiki Rais wetu amesaini, tunamsubiri na tunampongeza. Lakini Bungeni lazima mkataba huo pia uje sawa sawa na sheria tuliyoipitisha.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya ninakushukuru sana, ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuchangia katika bajeti ya Wizara hii ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Spika, bajeti ya mwaka 2020/2021 Mheshimiwa Waziri alieleza mafanikio makubwa sana juu ya bajeti hasa kwenye kipengele cha NIDA kwa asilimia 86. Kumekuwa na shida kubwa sana ya Vitambulisho vya Taifa hususan watu wa vijijini. NIDA walisema wana mpango wa kusajili watu takriban 25,000 leo hii Waziri anasema wamesogea wamefika watu 23,000 lakini waliopata Vitambulisho vya Taifa hawazidi milioni saba.

Mheshimiwa Spika, kuna watu walipata namba wakati ule akizungumzia bajeti hii walikuwa watu milioni 17 leo wameongeza wamekuwa 18. Deadline ya kupata Vitambulisho vya Taifa kwa mwaka huu ni tarehe 8 Juni, 2021 lakini kuna watu wanakaa zaidi ya mwaka mmoja hawajapata hivyo vitambulisho ijapokuwa wana hizo namba ambazo wamepewa hivyo kuwapa ugumu kuendelea kufanya shughuli za kitaifa kwa sababu wanavitegemea vitambulisho hivyo.

Waziri alisema kuna mashine mpya mbili wamenunua ambazo zina uwezo wa kutoa vitambulisho takriban 144,000. Naomba kupata maelekezo yake kama kweli mashine hizo zipo na vitambulisho vinapatikana. Leo Waziri ameeleza vizuri kwamba amejitahidi kutafuta taasisi zaidi ya 39 za umma na binafsi ili ziweze kujiunga na vitambulisho hivi vya taifa kama chanzo cha mapato ili watu waweze kutumia vitambulisho hivyo. Umuhimu wa vitambulisho ni mkubwa tunaomba Waziri atuambie mwisho wa changamoto hii ya upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa utakuwa lini.

Mheshimiwa Spika, nikija eneo la polisi, bajeti iliyopita walikuwa wajengewe nyumba 431 lakini leo hii tuna polisi wanakaa mitaani. Kamati imeshauri vizuri unapokuwa na polisi mtaani na yeye kazi yake anayoifanya wakati mwingine ni ya kugombana na hao raia kwa maana inategemea ni maeneo gani wanafanyakazi ni hatari sana kwa askari huyu. Polisi hawa wanakaa uraiani maana nyumba ni chache. Tunaomba bajeti hii waweze kuongezewa ili polisi wajengewe nyumba.

Mheshimiwa Spika, Rais amezungumzia suala la upandishwaji madaraja, naomba sana wakati huu madaraja hasa kwa askari wadogo utiliwe maanani. Hata hizo nyumba tulizozisema tuachane na viongozi wenye vyeo vikubwa kwani wanaopata shida ni maaskari wadogo ambao na wao wanahitaji kukaa kwenye makazi bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mafunzo ya kipolisi, nilishawahi kufika Chuo cha cha Polisi Kidatu, mazingira wanayosomea siyo rafiki kabisa. Majengo yale yalijengwa siku nyingi na ni chakavu, kwa hiyo, watu wale wanasoma katika mazingira magumu sana. Hivyo basi naomba Wizara hii safari hii isimamie na kuwatizama.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie makampuni binafsi ya ulinzi ambayo naamini yanasimamiwa na Wizara hii. Nataka kujua ni namna gani Wizara inasimamia hasa silaha za moto kwa makampuni haya binafsi. Wanawasimamiaje kuhakikisha wanatunza na kuwa waaminifu katika matumizi ya silaha hizi za moto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, makampuni mengi binafsi yanaajiri wafanyakazi toka nje ya nchi. Ukienda kwenye hoteli nyingi za Five Stars, Three Stars utakuta walinzi wale wengi wanatokea Kenya wakilinda kwenye makampuni haya. Mimi nafikiri ni wakati sasa kuhakikisha SUMA JKT wanapewa kazi ya kulinda mahoteli hayo badala ya kutumia makampuni binafsi kwa sababu vijana wetu wengi hawana ajira, tunafikiri wao wanaweza wakatusaidia kupunguza ajira kwa kutumia makampuni ya nyumbani na si vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie masuala ya Zimamoto. Mara nyingi huwa nasema hapa Zimamoto ni jeshi la mwisho. Nikisema la mwisho nina maana hii, ni kweli kabisa ukiangalia uniform, dawa na nyumba za Zimamoto ni jeshi ambalo limekuwa likipata bajeti ndogo kulinganisha na majeshi haya mengine. Kama Kamati ilivyosema tunahitaji kuwekeza kwenye Jeshi hili. Si hivyo tu wamezungumzia Jengo la Mchicha shilingi bilioni 2 ziliwekezwa pale, ile ni pesa iliyolala mahali pale, najua hapa tumekwishajenga lakini bado kuna haja ya kuongeza fedha na kuhakikisha lile jengo linaisha hata tukalipa matumizi mengine.

Mheshimiwa Spika, suala la magari, bajeti iliyopita walisema watapata magari matano kutoka Nyumbu. Naomba Mheshimiwa Waziri aniambie kama magari hayo yamepatikana kwa kutoa taarifa mahali hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, magari ya Zimamoto, mikoani hakuna magari na kama yapo wafanyakazi ni wachache. Tunaomba ikama ya wafanyakazi katika idara hii iongezwe.

Mheshimiwa Spika, nikienda Magereza, leo hii watu walioko magerezani wafungwa ni nusu na mahabusu ni nusu. Tulisema wakati uliopita ni bora kukawa kuna kesi zile ambazo zinapunguza idadi ya mahabusu ili tuweze kupata nafasi ya kuwaweka wafungwa kwenye nafasi ya kutosha. Kama wafungwa ni zaidi ya milioni iliyotajwa, nusu 16 ni wafungwa waliohukumiwa na nusu 16 ni mahabusu. Kwa hiyo, mahabusu ni wengi tunaomba kesi zifanywe haraka haraka ili kusudi hawa mahabusu waweze kutoka na magereza yaweze kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kimsingi magereza mengi ni magereza yaliyojengwa enzi za ukoloni. Mimi sipendi watu wetu wafungwe lakini wafungwe katika staha, wakae kwenye magereza ambayo yana vyoo vya kutosha na wanawake waliokuwa kule magereza wapate stara ya kutosha. Tukiwa na magereza yenye maeneo madogo kama ni mahabusu kisaikolojia unakuwa umeshamfunga.

Mheshimiwa Spika, tumesema magereza itengeneze chakula. Gereza la Songwe ni kubwa na lina ekari nyingi lakini hawana vifaa vya kuwawezesha kulika. Ili ulime na uzalishe chakula lazima uwe na matrekta, wataalamu na fedha ya kununulia mbegu. Mmesema mmetenga mbegu lakini ni lini zitapatikana kwa sababu kila mwaka mnazungumzia kutenga mbegu. Songwe wana eneo kubwa lakini hawana trekta, vifaa vya kutosha na wataalamu, naomba Wizara itazame suala hilo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Sophia.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami nikuunge mkono kwenye eneo la Wizara kusimamia gharama za uchimbaji au gharama za miradi. Mheshimiwa Waziri na timu yako kama walivyosema wenzangu mnafanya kazi nzuri sana, lakini kule wilayani na mikoani lazima timu yenu pia ishuke ihakikishe inasimamia miradi yote ambayo Serikali imetoa fedha. Tuna mradi wa maji Masukuru, tulilalamika tukasema kwamba mradi ule ulifanywa chini ya kiwango. Nasisitiza kiwango ni kitu cha muhimu sana kwa sababu pesa ikitolewa ni lazima ifanye kazi sawasawa na thamani ya pesa iliyotolewa.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie juu ya Wizara hii hasa walipoanzisha Jumuiya ya Maziwa kwa maana ya Ziwa Nyasa, Ziwa Tanganyika na mengineyo mmefanya kitu kizuri. Mkoa wa Mbeya una vyanzo vingi vya maji lakini tukitumia Ziwa hili la Nyasa kama ambavyo mmefanya Ziwa Victoria mtakuwa mmetatua tatizo kubwa sana la maji katika Mkoa mzima wa Mbeya wenye majimbo saba. Nafahamu ni fedha nyingi lakini tutakuwa tumetatua tatizo la muda mrefu la wananchi wetu kukosa maji sehemu za Nyanda Juu Kusini na maeneo ya Mbeya jambo ambalo sio sahihi kabisa kwa sababu tayari tunavyo vyanzo vya maji vingi lakini mpaka leo miaka 59 ya Uhuru hatujapata maji ya bomba maeneo mengi sana. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri kwa weledi mlio nao msimamie fedha za Serikali kama alivyosema Mheshimiwa Spika kwamba Wizara hii mnapata fedha za misaada na mikopo tatizo ni mipango na viapaumbele ambavyo ni vyema tukavisimamia.

Mheshimiwa Spika, ukienda katika Wilaya ya Rungwe kuna maeneo ambayo kama nilivyosema yana vyanzo vingi vya maji lakini ukienda maeneo kama ya Kimbira hukuti maji, ukienda sehemu za masoko au sehemu za Buliaga ambako ni mjini kabisa utakuta maji ni shida. Si hivyo tu watu wengine wanapata maji lakini bili za maji zinapokuja pia ni tatanishi. Kuna wakati unaenda kulalamika kwa nini bili yangu mimi nalipa hela nyingi wanakuambia tumekosea, sasa hii ni kwa wale ambao wana uwezo wa kwenda kufuatilia. Kwa hiyo, tunaomba wanaosimamia mambo ya bili na utoaji wa maji maeneo kama hayo uwe wa vigezo vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niliwahi kusema hapa Bungeni kwamba kuna maeneo yanakuwa ni vyanzo vya maji, kwa mfano kwa kule Rungwe sehemu za Mpumbuli na Kasyeto, wao wana chanzo cha maji lakini cha kushangaza mabomba yanapita kama alivyosema Mheshimiwa Tunza wao hawana maji yanaenda sehemu za Ushirika na sehemu zingine wale wenye chanzo cha maji hawapati maji. Nafikiri hatuwatendei haki Mheshimiwa Waziri, najua labda ulikuwa hauna taarifa nakutaarifa sasa kwamba tunahitaji watu wa Kasyeto na wao wapate maji maana chanzo cha maji kinatoka kwao.

Mheshimiwa Spika, suala la ukosefu wa watendaji kazi, nimeona hapa katika hotuba ya Waziri wana upungufu wa wafanyakazi 1,500 na kuendelea. Tunahitaji watu hawa wapate watenda kazi ili kusudi iwe rahisi kuwafikia watumiaji wa maji. Tunaona wakati mwingine hata bili zinachelewa kusomwa kwa sababu anayesoma bill labda ni mmoja kwa eneo kubwa la sehemu husika. Kwa hiyo, mtakapokwenda kuomba watumishi iwape kipaumbele ili kuleta ufanisi katika utendaji wa kazi wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukweli maji ni uhai na ukimtua mama ndoo kichwani unakuwa umesaidia uchumi wa Taifa kuongezeka. Muda mwingi wanawake wanautumia kwenda kufuata maji mbali na kupoteza muda wa kutafuta pesa kwa ajili ya familia. Kwa hiyo, tunaamini Mheshimiwa Aweso na timu yako mkifanikiwa kusaidia kutatua tatizo la maji mtakuwa mmesaidia Tanzania kuwa ni nchi ya kati katika uchumi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, naomba niendelee kuipongeza timu nzima ya Wizara ya Maji lakini pamoja pamoja na pongezi nyingi tunataka mama atuliwe ndoo kichwani maisha yaendelee. Ahsanteni sana. (Makofi)


Hoja Kuhusu Bei ya Kuuza na Kununulia Mahindi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia hoja hii. Wazo la Serikali la kuwa na vituo hivi ni la muhimu na ni la msingi kwa ajili ya faida ya mkulima wa chini kabisa. Lakini vituo hivi vya NFRA viko vichache, na mwendo wa mkulima kutoka kata moja kwenda sehemu ambayo wameweka kituo ni mbali sana na hivyo kuongeza gharama katika ununuzi wa mazao hayo. Kwa mfano, mkulima anabeba mahindi anapeleka zaidi ya kilometa 100 kwenda kuuza; obvious ile bei ya shilingi mia nane itamkata mkulima. Kwa hiyo tunaomba vituo viongezeke viwasogelee sehemu ambapo wakulima wapo.

Mheshimiwa Spika, lakini mbili wale wauzaji ambao Mheshimiwa Bashe ni watendaji wako kule chini wengi sio waaminifu wanaenda kusema mahindi haya hayafai ni reject lakini wakati huo huo wanaenda kuuziwa wao pembeni nakuja kuuza ndani. Of course hili suala linahitaji utafiti wa kiintelijensia ili uweze kuhakikisha hilo suala, kwa sababu leo mkulima kabeba mahindi kilometa zake tano, sita amepeleka kwenye kituo mnunuzi anasema mahindi haya hayafai.

Hilo nililisema hata kwenye parachichi haya, lakini usiku watu wachache, wajanja, madalali wananunua na tena wanayapeleka kwenda kuyauza kesho yake. Tunaomba uangalizi wa karibu uwepo na kuhakikisha maadili yanakuwepo kwa wale wanunuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, hili ni soko huria, tunaomba wananchi wapewe uhuru wa kuuza. Nimelima mahindi yangu, nahitaji kumpeleka mtoto shule, nikauze ninapotaka mimi, baadaye itatusaidia sisi kuweza kujua bei itakuwa juu na mkulima atajisikia vizuri akiuza anapotaka. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nitaanza na suala la TAZARA. Toka waasisi wa nchi yetu na nchi ya Zambia waunde TAZARA ni zaidi ya miaka 46 sasa. Waliunda kwa Sheria Na. 23 ya mwaka 1975.

Mheshimiwa Naibu Spika, TAZARA imekuwa na matatizo ya kifedha kwa muda mrefu sana. Imeshindwa hata wakati mwingine kutoa mishahara na kwa wanaostaafu kwa wakati. Ninaiomba Serikali iweze kuwekeza fedha zake kwa watu wa TAZARA ili iweze kujiendesha. Tunajua kabisa TAZARA – na kama ulivyosema hapo awali, inasaidia Nyanda za Juu Kusini ambao sisi ndio tunaozalisha mali nyingi, na hasa chakula katika Taifa hili. Sasa tukiwekeza kwenye reli hii itasaidia sana upatikanaji wa chakula hata kwa Dar es Salaam na kwenda huko huko Zambia ambako tunapeleka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, natoa ushauri; kwa sasa tunajua kabisa barabara zetu zinaharibika kwa sababu ya shaba inayobeba toka Zambia kuja kwenye Bandari ya Dar es Salaam. Sasa iwekwe sheria kama ikibidi, watu wa Zambia wapitishe shaba hiyo kwa kutumia reli hii ili iweze kupata fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, wenzetu wa TAZARA ya Zambia wameacha na kuweka nguvu zaidi kwenye reli hii, wametuachia sisi wenyewe. Hivyo basi, tunaomba tuisaidie reli hii iweze kufanikiwa na hasa kupata fedha ya kulipa mishahara na kujiendesha mpaka hapo itakaposimama yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua TAZARA ina majengo katika stesheni zote, ina majengo pale TAZARA Makao Makuu, lakini bado wanashindwa hata kuweza kuitengeneza. Tunahitaji tuipatie fedha zaidi. Kama tuna miradi mipya ya SGR tumeanzisha, tunaweza tukawekeza katika TAZARA nayo ikaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie TANROADS. Kwenye ripoti ya CAG; wamesema TANROADS ilishindwa kutoza tozo ambayo ilikuwa ni zaidi ya shilingi bilioni tano kwa watu wa Sanzali ambayo ilikuwa ni barabara ya kilometa 50. Sasa hili ni tatizo. Kama tunashindwa kufanya tozo, tunawezaje kupata mapato kama Taifa? Kwa hiyo, nawakumbusha watu wa TANROADS kuwa makini kusimamia shughuli ambazo tunawapatia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Daraja la Kigogo na Busisi lilianzishwa kabla ya cheti cha kuangalia madhara ya kimazingira. Walianza ujenzi kabla ya kupata kile cheti. Tunawaomba sana wasifanye chochote mpaka wawe wametimiza haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tumezungumzia daraja lile la Jangwani, bado mpaka leo hii wanasema kwamba wanaendelea kuangalia upembuzi yakinifu na mambo kama hayo. Tunaomba wafanye haraka ili Jangwani isiendelee kuzama na watu waendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado kuna shida ya pesa ya maendeleo. Tunapitisha sisi kama Bunge, tunasema tunatoa fedha hizi, lakini mwisho wa siku bado fedha hizo haziendi kwenye Wizara husika. Leo hii Kamati imetoa maoni pale, kwamba miezi minne imebaki fedha ziwe zimekwisha, lakini bado hawajaletewa fedha zote. Tumeona nyingine ni asilimia 30, nyingine asilimia 50; hatuwezi kufanikiwa kama hatutoi fedha na maendeleo yakaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba ujenzi wa viwanja vya ndege vile vya kimkakati. Kwa mfano, Viwanja vya Ndege vya Songwe, Moshi, Manyara na Iringa, hivi vimewekwa kwa ajili ya utalii, lakini bado havijaanza kuwekewa mkazo wa kujengewa pale. Tukija Uwanja wa Ndege wa Songwe, mpaka leo taa hazipo kwa hiyo, ndege haiwezi kuondoka usiku. Kwa hiyo, tunaomba waziweke hizo taa, maana ni muda mrefu tumekuwa tukilizingumzia suala hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, madeni ya wananchi ambao wamepisha ujenzi wa viwanja vya ndege, tunaomba walipwe kwa wakati. Tunaomba tafadhali kwa sababu wananchi wanajitolea kwa ajili ya kuweza kusaidia maendeleo ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia barabara za mikoa zinazounganisha vipaumbele kwa ajili ya maendeleo mbalimbali, kwa mfano, Kyela kuna barabara ambayo inaunganisha Kyela na Ileje, ile ni barabara muhimu sana. Tunafahamu Ileje kwa kupitia Mbeya ni mbali lakini wakijenga ile barabara ya Ileje kuelekea Kyela itatusaidia sana kufanya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado ninajua kwamba kuna shida ya vibali TRA. Pale barabara zinapojengwa TRA wamekuwa wakichelewa kutoa ule msamaha wa kodi na hiyo husababisha barabara zinapojengwa zinakuwa zinachelewa na kuleta deni kwenye Serikali yetu. Ninaomba waweze kusimamia hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninaomba niishie hapo na huo ndiyo mchango wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Wananchi miaka ya nyuma ilikuwa inaonesha hali nzuri sana katika hali za michezo. Tunajua michezo inatambulisha Taifa, kwa hiyo, nilikuwa ninaomba Jeshi hili liendelee kuhimiza wanamichezo jeshini waweze kuisaidia Tanzania. Tunakumbuka kina Nyambui waliitambulisha Tanzania vizuri sana nyakati zile, sasa hivi mimi kama promoter wa ngumi tuna wachezaji watatu tu kutoka jeshini. Tuna wanangumi watatu wanatuwakilisha nje ya nchi kutoka jeshini, sasa Jeshi haliwezi kutupa wanangumi watatu, tunaomba muongeze wachezaji wa ngumi maana ngumi inalipa na inatambulisha Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kumtambua Suleiman Gariatano ambaye ni mwanajeshi anatuwakilisha vizuri, Suleiman Kidunda anatuwakilisha vizuri, Bonabuchi anatuwakilisha vizuri, lakini JKT ina msichana Mnyakyusa mwenzangu Grace Mwakimere naye ni mpiga ngumi mzuri sana. Ninaomba tusimamie michezo ya ngumi Jeshini maana itasaidia kuisaidia Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye nyumba za wanajeshi. Mimi nimezaliwa kwenye Kambi ya Jeshi nyumba za jeshi kwa mfano quarter zile za Keko mpaka leo zimechaka, ukienda nyumba za Mwenge pale Mwenge magorofa ni chakavu sana. Ninashukuru kwamba mmejenga mwaka 2025 mpaka mwaka 2020 mmejitahidi sana kujenga nyumba, lakini zile za zamani mmeziacha kuzikarabati. Ninaomba bajeti hii muweze kuzikarabati wazazi wetu waweze kuendelea kukaa katika mazingira mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia suala la maduka yale ya bei nafuu yaliyokuwa jeshini, yalikuwepo kwa muda mwingi mpaka sisi tunakua yalikuwepo, lakini miaka sita iliyopita yalisitishwa. Ninaomba yarudishwe kwa sababu wazazi wetu hawa na wanajeshi wetu na makamanda hawa hawana muda wa kufanya biashara zingine. Kwa hiyo, mkiwapa eneo la kwenda kununua vitu bei rahisi mnakuwa mmewasaida na kuwapa motisha. Tusiwaache tu wakaishia kufuga bata na kuku kwenye quarters zetu. Tunaomba warudishiwe yale maduka ili waweze kupata vitu kwa bei rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia suala la upandishwaji vyeo hasa wanawake, ninajua Waziri wewe ni mwanamke, ninaomba utazame wanawake makamanda, ambao bado wako Jeshini wanaofanya kazi vizuri wapandishwe vyeo kwa haraka. Najua hatupandishi cheo kwa sababu ni mwanamke, ninafahamu, kwa sababu, wako jeshini ni makamanda ninajua wana uwezo wa kupandishwa vyeo na wana uwezo wa kufanya kazi yao vizuri.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo suingi hoja, aah naunga hoja. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana na mimi kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu. Mimi nitazungumzia suala la hati za kambi za jeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyojua mimi kwa uzoefu mdogo kwa sababu nilikuwa mtoto wa quarter ninajua kambi nyingi za jeshi zilianza kuwepo, lakini kwa kutokuwa na hati za kumiliki ile ardhi watu wanaingia, mwisho wa siku inaonekana kwamba, jeshi limewavamia wananchi au wananchi wamelivamia jeshi. Kwa hiyo, mimi nilikuwa ninaomba Serikali iweze kujipanga na ninajua pale jeshini kuna wasomi waliosomea wanaweza kujipimia wenyewe bila kutegemea Wizara ya Ardhi, mambo mengine yakafanywa baadaye, lakini angalau wakajipimia wakajua maeneo yao ni yapi wanayoyamiliki, ili iweze kuondoa migogoro mbalimbali ambayo inaonea majeshi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba jeshi siku zote lilikuwa linakaa mbali na wananchi na linakuwa na square meter nyingi, lina square meter nyingi kwa ajili ya kumiliki lile eneo, lakini usipopima mtu akaja akajenga mwisho wa siku mwenye hati ndio mwenye mali. Hivyo basi, tunaomba Wizara na ninajua Mheshimiwa Kwandikwa kwa kuja kwako unaweza ukahahakikisha mnapata fedha za kupima kambi za jeshi nchi nzima na kuweza ku--identify maeneo yenu kwa usalama zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia wanawake katika jeshi, leo hii Mheshimiwa Waziri ametuletea Majenerali tumewaona tunashukuru, lakini bado tuna haja ya kuongezewa vyeo kwa wanawake zaidi jeshini, hasa kada za chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua wanawake wanaweza, sasa katika wote hatujajua ni wangapi, hatuna statistics kama Bunge tulioletewa kwamba wanawake wangapi ambao wana vyeo hivyo. Sawa leo wamekuja majenerali tunawapongeza na tumeyasema haya mwaka jana na mwaka juzi na miaka iliyopita, lakini bado kada ya masajenti na kuendelea mpaka makapteni waongezeke zaidi wanawake ili waweze kuongezewa vyeo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia nyumba za askari; nimesema mimi nimezaliwa kambini; kiukweli kwa mfano flats za pale Keko njia panda ya kwenda uwanja wa Taifa tumehamia pale mwaka 1973, lakini mpaka leo hii maghorofa yale hayajawahi kupakwa rangi. Tunaomba tafadhali Mheshimiwa Kwandikwa pamoja na kwamba, maghorofa mengi yamejengwa kwa ajili ya askari, tunaomba ukarabati wa nyumba za askari uendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si tu hivyo, bado askari wa rank za chini wanaishi uraiani. Unapokuwa na wanajeshi wanaokaa uraiani kunakuwa hakuna udhibiti wa wale askari kwa sababu hawa watu wanaweza wakaitwa wakati wowote kwa ajili ya kwenda kufanya kazi yoyote kwa muda wowote. Anapokuwa na mama mwenye nyumba mwenye funguo za geti anakaa nazo chumbani, hii si sawa tunaomba jeshi lijenge nyumba zaidi hasa kwa askari wadogo waweze kupata makazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazungumzia habari za upandishwaji wa v eo nimeshalisema, lakini mwisho wa siku ajira kwa wanajeshi. Tumeona Kamati ya Nje, Ulizni na Usalama (NUU) imezungumza hapa kwamba kuna upungufu wa wafanyakazi jeshini, tunaomba sana ikama inayosimamia wafanyakazi jeshini waweze kuajiriwa. Na tunao vijana wa JKT wengi ambao wamemaliza JKT, kama ni kigezo cha kwenda jeshini basi wachukuliwe vijana wetu hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiondoka kwenye jeshi nikaingia kwenye JKT. Leo hii JKT ina vijana wengi sana walinzi, ametoka kuongea Mbunge mchana wa leo kwamba JKT haifanyi tender, mimi sikubalini. Ninaamini katika JKT kupewa malindo mbalimbali katika Taifa hili, tunaogopa sana kuwa na walinzi kwenye benki, kuwa na walinzi kwenye kampuni za kiserikali na mashirika ya umma kutoka nje ya kampuni binafsi. Tunatamani JKT iajiri vijana wengi zaidi kwenye kampuni hizi, lakini shida kubwa iliyopo kwa JKT wanawalipa mshahara mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata wewe mwenyekwe ukiwa unaelekea Mbeya ukipita pale kwenye Bwawa letu la hapo Mtera utakuta vijana kwenye mazingira magumu, mishahara wanayoipata ni midogo. Tunaomba sana kwa sababu unapokwenda kumnunua mlinzi kwenye kampuni unaweza ukawa unapewa laki tano kwa askari mmoja, lakini wale vijana mshahara wanaoupata ni chini ya shilingi 200,000 tunaomba muwaongezee mishahara kusudi wafanye kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia JKT hao hao wenzetu sasa wanafanya mambo mengi ikiwemo mambo ya maji kuna mmoja amasema wafanya mambo makubwa zaidi, lakini sio vibaya kuanza na madogo ili uende kwenye makubwa. Mimi ninashauri mradi wa maji kutoka JKT mashirika yote ya umma, Wabunge na maeneo mengine yote yanayohusiana na Serikali tusitumie maji ya mashirika ya watu binafsi, tulazimishe tutumie maji ya JKT kama kuwasaidia wala msishituke kwa sababu tunataka kuisaidia JKT ili iweze kutoa ajira kwa vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuelezea suala la Kiwanda cha Nyumbu; wenzangu wengi wameelezea na mimi ninaamini kuna fedha nyingi wamekwisha kupata tunaposema Tanzania ya viwanda tunataka Jeshi letu kwa sababu wao wana dhamana kabwa kwetu tuwekeze fedha nyingi kwao waweze kuzalisha. Nyumbu kama walivyosema waliotangulia ni sehemu ambayo ingekuwa mfano, waliwahi kutengeneza gari, wanatengeneza magari ya zimamoto, tuwekeze fedha ili waweze kutuzalishia zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo siungi hoja, nasisitiza fedha ziongezewe na zile zilizopangwa ziweze kuwafikia wahusika, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii. Kimsingi kwa sababu Rais sasa ni mgeni na hii ndio bajeti yake ya kwanza, niseme tu tunatoa ushauri kwa Serikali, yale ambaye yalikuwa yakikosewa awamu zilizopita, tunaomba bajeti hii wasiendelee kuyakosea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama wengi walivyosema, tunazungumzia TRA ambayo sisi kama Watanzania tumeipa jukumu la kuweza kukusanya kodi kwa niaba ya wananchi wote. Leo hii TRA, imeshindwa kukusanya kodi sawasawa na malengo ambayo sisi tuliwapangia wakusanye kodi. Tunafahamu kabisa bajeti yetu ni ya kukusanya kodi na kutumia. Kwa hiyo wanapokosea na wanapofanya chini ya kiwango cha ukusanyaji kimsingi inachelewesha maendeleo ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TRA wana uhaba wa wafanyakazi na mtu anayesimamia TRA, kwa TRA iliyopita kuna wakati tuliona walichukua hata vyombo vya usalama kusaidia kukusanya kodi. Watu wa TRA wanatakiwa wasomee na ndio maana kuna Chuo cha Ukusanyaji wa Kodi. Tunaomba sana, TRA iwajengee uweze wafanyakazi wake wa ukusanyaji wa kodi na hasa hasa kupata mafunzo ya mara kwa mara ili wawe makini na wawe na weledi katika ukusanyaji wa kodi. Mlipakodi ni mtu namba moja anayefanya nchi hii iendelee, ukimwendea kibabe, ukamwendea kwa hali za vitisho, walipakodi wengi wanajificha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado TRA haijaweza kufanikiwa walipa kodi ni akina nani, wachache wanaowafahamu hao ndio wanao wabana zaidi. Namwomba Mheshimiwa Waziri tuhakikishe TRA inafanya identification ya walipakodi wa Nchi nzima ili kodi iweze kulipwa kwa usahihi na ufasaha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ukaguzi wa CAG wa mwaka 2019/2020, CAG anasema katika wale watu ambao wamekwepa kodi na Baraza ya Kodi tunadai kodi zaidi ya trilioni 360. Hii ni nini? Ni kwamba bajeti ya nchi hii zaidi ya miaka mitano inaweza ikajengewa uwezo kutokana na fedha hii ambayo inapotea kwa wale watu ambao hawalipi kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Mabaraza ya Kodi ambao wao wanatakiwa wafanye kazi kesi kwa sisi tunaowadai, TRA haijafanya kwa ukamilifu. Pesa hii trilioni 360 na Mheshimiwa Rais anisikilize, tunahitaji kuhakikisha TRA inasimamia fedha hizi ili ziende kuongeza maendeleo ya nchi hii; kwa sababu leo hii tunakusanya fedha kidogo, bajeti yetu ya mwaka mmoja ukijumlisha hizi trilioni 360 ni miaka kumi takriban tunaweza tukakaa tunakula pesa ambayo ipo mikononi kwa watu haijakusanywa sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nini tufanye? Kwanza kabisa nimesema lazima wafanyakazi wajengewe uwezo, hicho ni cha msingi. Pia Ikama ya TRA ina wafanyakazi wachache sana ambao hawajaweza kuajiriwa na kutusaidia kukusanya kodi. Ni aibu sana watu wanaokusanya kodi eti wana uhaba wa wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji kabisa kwenye ile Mamlaka ya Rufani ambayo ndiyo nimesema wao wanao wajibu wa kufanya hizo kesi lazima tuwaongezee nguvu waweze kufanya kesi za ukusanyaji wa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumzie wafanyabiashara. Leo hii kwenye biashara ili ufungue biashara kuna tozo nyingi sana na ziko scattered. Lazima tuwe na one stop center ambayo mfanyabiashara akitaka kufungua biashara yake ahakikishe anakwenda anakutana na OSHA sehemu moja, akutane na watu wa mamlaka ya halmashauri sehemu moja, sio kwamba anakaa mwezi mzima kwenye dirisha moja akifuatilia namna gani afunguliwe biashara. Akimaliza hapo tena unamtuma aende OSHA, akitoka OSHA anakwenda kwenye halmashauri anakutana napo kuna tozo, hii inaleta usumbufu kwa wafanyabiashara. Tunaomba wawe na eneo moja, mtu akiamua kufungua biashara isiwe ni mateso, kazi yake iwe kutafuta mtaji wala siyo kuhangaika namna ya kufungua biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la kilimo. Asilimia 65 ya Watanzania wanategemea kilimo, lakini leo hii nikizungumzia Nyanda za Juu Kusini ambayo ipo kwenye big five ambayo inalisha Taifa hili, leo hii hatuna mkakati makini kwenye kilimo hususan kwenye utafiti. Leo ukienda Mbeya kuna Chuo cha Uyole, huu ni mwaka wa tatu hawajapata fedha za utafiti. Huwezi kuwa na kilimo bila ya utafiti. Ni lazima uwekeze kwenye utafiti ili ujue udongo huu unafaa mbegu gani, ili ujue mazao haya yanafaa maeneo gani, lazima watafiti watutangulie. Kama kilimo kinachukua asilimia 65 ya Watanzania, tunahaja ya kuwekeza maeneo hayo ili tuweze kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii bajeti ya kilimo inakwenda chini ya asilimia 30. Huwezi kupitisha bajeti kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania utekelezaji wake ambao Wizara ya Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Mheshimiwa Waziri haipeleki fedha kwa wakati na inapeleka chini ya kiwango. Hatuwezi kufanikiwa, kwani kilimo ndio kila kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukizungumzia kilimo, tunazungumzia masoko, vitu hivi vinakwenda sambamba. Leo hii katika Nyanda za Juu za Kusini tumekuwa wakulima wazuri wa parachichi. Tunaita ni zao la kijani, zabibu ya kijani, lakini leo hatujajua yakini wanunuzi wa parachichi waliowekeza huko Iringa, Njombe, Rungwe, na maeneo kama haya wanauza kiasi gani nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wananunua kwa kilo moja 1,500 sisi unafahamu tulikuwa tunauza maparachichi 10 kwa buku, lakini leo wanachukua kwa 1,500 kwa kilo, lakini bado kuna haja ya kuchunguza, kama mwekezaji ananunua parachichi, amesafirisha zaidi ya container 100 yeye kapata kiasi gani? Kwa maana ukienda nje, unakuta parachichi moja unaweza ukapata kwa dola 1.9 ambayo hiyo ni karibu Sh.3,000 kwa nini mkulima asiuze kwa bei kubwa 1,500 bado naona ni ndogo, naomba Mheshimiwa Waziri Mwigulu asimamie hilo ili wakulima wetu wapate fedha sahihi na sawasawa na thamani ya zao lao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia masoko nikija suala la chai. Nimekuwa nikizungumza sana suala la chai katika Bunge hili. Hii leo, chai inanunuliwa dunia nzima na kwenye soko la dunia bado ina soko. Katika nchi hii, ukienda Rungwe chai ni Sh.320 baada ya kupiga kelele. Ukienda Njombe chai Sh.500, ukienda Lushoto chai iko juu, mimi nataka kujua Mheshimiwa, Bodi ya Chai ni moja, nchi ni moja na CCM ndio wanaongoza nchi hii, kwa nini kunakuwa na bei tofauti wala hakuna usawa wa bei katika zao moja? Naomba suala la chai lipatiwe jibu makini wakati Mheshimiwa Waziri anapokuja kujibu masuala yake hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la maji. Maji ni uhai, tunafahamu kabisa kwamba maji ndio kila kitu, lakini leo hii, tuna vyanzo vingi vya maji na nijikite kwetu Nyanda za Juu Kusini. Leo hii ni aibu kubwa sana miaka 59 kwenda 60 ya Uhuru hatuna maji ndani ya nyumba za watu tunachota maji mitoni na vyanzo vya maji. Ziwa Nyasa lipo kama ambavyo Ziwa Victoria lipo. Niiombe Serikali iweze kuwekeza kwenye Ziwa hili na tuweze kupata maji katika Mkoa wa Mbeya wote, tupate maji kwa sababu uwezekano wa kupata maji upo na fedha zipo za kuweka maji. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango huu. Nimeona Wabunge wanzangu wengi wamezungumzia suala la kilimo, bado na mimi nitaendelea kujikita hapo kwa sababu bado nchi yetu kwa asilimia zaidi ya 65, watu wetu wanategemea kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo taarifa ya Kamati imesema, Kamati imeongea vizuri sana na imetoa maoni mazuri sana kwa Serikali, kilimo kwa asilimia zaidi ya 26 ndio inaongoza katika pato la Taifa, lakini cha kushangaza inakuwa kwa asilimia tatu mpaka nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema asilimai 65 ya watu ni wakulima bado, leo hii pesa ya maendeleo ya kilimo bilioni 200 karibu ambazo zinatengwa 294 kwa kweli ni ndogo na Kamati imeshauri imesema ni bora pesa hiyo ikaongezeka angalau ikafika bilioni 450 ili kuweza kuisaidia Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu wakulima wetu wengi sana wanajitegemea na kikubwa zaidi ambacho kinawatesa ni ukosefu wa pembejeo, ukosefu wa Wagani na watu ambao wanaweza kusimamia kazi za kilimo. Tunaomba Serikali iweze kuona umuhimu wa kuleta ruzuku kwenye mbolea. Tunaona sasa hivi hasa Nyanda za Juu Kusini ambao sisi tunalisha almost nchi nzima, leo hii kilimo bado hakijaanza kwa sababu watu wanatafakari namna gani wataendelea kulima kwa sababu mbolea zimepanda bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viongozi wa kilimo kwenye wilaya ni wachache, leo hii Serikali haijaajiri kwa muda mrefu Maafisa Ugani na waliopo hawana vifaa vya kuweza kuwasaidia kutenda kazi. Majimbo ni makubwa na maeneo wanayofanyia kazi ni makubwa wanashindwa kuwafuatilia wananchi na kuhakikisha wanatoa mazao kama inavyopaswa. Sasa kumetokea kuna watu binafsi wanaoingia kwenye mambo ya kilimo na kuwadanganya wakulima. Naamini wewe umesikia na Wabunge wenzangu wamesikia, sehemu za Njombe kuna watu wamesema kuna mazao ambao wananchi wakiyalima watapata mapato mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna zao hili la vanila, watu wametoa fedha kwa makampuni binafsi wamelima hizo vanilla, wamedanganya kilo moja ni milioni moja na mwisho wa siku hawajapata hicho ambacho walichetegemea. Serikali ilikuwa na wajibu wa kuweka Maafisa Ugani ambao wao ndio wangekuwa waanawaambia wakulima na wala sio watu binafsi, mwisho wa siku wanawadanganya. Tunahitaji kuongeza nguvu kwa watu wetu ili kilimo kiweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masoko ya mazao ni shida, leo hii kilimo cha chai katika Wilaya ya Rungwe na Mikoa ya Njombe bado chai inauzwa kwa bei ndogo sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu amejitahidi kufika maeneo yetu na tumelalamika muda mrefu, lakini bado bei inasuasua, wakati bei ya soko la dunia bado iko juu, hatuelewi kwa nini watu wetu hawapati soko la chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ndizi zinazalishwa kwa wingi sana. Leo hii kuna nchi kama za Jamaica wanaishi kwa sababu ya ndizi, leo sisi tuna ndizi tunalima na watu wetu wanalima mwisho wa siku ndizi mkungu mmoja shilingi elfu mbili. Naomba Wizara husika isimamie kuhakikisha zao hili linakuwa zao la kibiashara vinginevyo wanaingia wafanyabiashara wale ambao tunasema ni wachuuzi, wananunua kwa kuwalangua wakulima kupeleka ndizi Malawi, kupeleka ndizi Zambia, wakati huo wanapata wao faida, lakini mkulima wa Wilaya ya Rungwe au Mkoa wa Mbeya hapati faida yoyote. Tunaomba Wizara isimamie hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru kwa zao la cocoa tunafahamu kuwa cocoa ni zao ambao lkinaleta faida katika dunia na Tanzania nafikiri cocoa yake ni bora, ya pili kwa maana baada ya Ghana inafuata Tanzania. Tunaomba Wizara hii na hasa Mheshimiwa Bashe najua anajitahidi, lakini kwa hili tunahitaji cocoa iongezeke bei kutoka elfu tano ambayo imepanda msimu huu, iende mbele zaidi maana soko la dunia cocoa ina bei kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri Serikali ina haja ya kuongeza fedha kwa watu wanaonuna NFRA, wanaonunua mazao. Kwanza kabisa capacity ya kubeba mazao hawana kwa sababu hawana maghala mengi katika maeneo mbalimbali. Naomba Serikali iijengee uwezo taasisi hii na hasa wakati wa msimu wa kununua mazao pia wawe na pesa za kutosha waweze kununua mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoke hapo kwenye kilimo niende kwenye eneo la miundombinu. Reli ya TAZARA ilianzishwa kati ya muungano wa nchi mbili, lakini sheria iliyoanzisha reli ya TAZARA nafikiri ina upungufu kwa sasa. Tunaomba Serikali sasa ilete marekebisho ya sheria ya reli hii ili kusudi Tanzania iwekeze kwa wingi fedha zake kwenye reli hii, maana ina faida kwa Nyanda za Juu Kusini ambapo mazao mengi yanazalishwa kule. Naomba Serikali ifanye hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naenda kwenye sekta binafsi, sekta binafsi inasaidia sana uchumi wa Taifa letu, lakini kumekuwa na mlolongo mrefu sana kuisaidia sekta hii. Naomba Serikali iangalie makosa madogo madogo ambayo yanasababisha sekta binafsi isifanye kazi yake vizuri. Kuna urasimu mkubwa wa usajili wa makampuni mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tozo zipo nyingi, unakuta mfanyabiashara anapotaka kufungua biashara tozo zipo sehemu nyingi nyingi na zinachukua muda mrefu, anaenda kwenye dirisha moja inamchukua wiki mbili, akienda sehemu nyingine muda umekwenda, mwisho wa siku hata wawekezaji tunaowaita waje kuwekeza nchini inabidi waende nchi jirani kwa kuwa sisi tuna mambo mengi sana ya ukiritimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kabisa nchi yetu inazungukwa na nchi mbalimbali, na tunafahamu – siwezi kuitaja hiyo nchi – lakini hiyo nchi inasubiri sisi tukosee ili wao waondoe yale ambayo sisi tunayaweka kama vikwazo na kuwakaribisha hao watu waende kwao na sisi tunakosa wawekezaji. Ninaamini Serikali imekuwa ikitamka sana suala la uwekezaji na kuwaita wawekezaji wengi wafike lakini mwisho wa siku hatuna ufanisi katika kuwakubalia hao watu na kuwasaidia ili waweze kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sekta binafsi hii wanapotaka kupata mikopo kuna usumbufu mkubwa sana wa upatikanaji wa mikopo. Tumekuwa tunahangaika na kusema kila siku na riba, na wenzangu wametoka kuzungumza hapa kwamba riba zimekuwa kubwa sana. hatuwezi kusaidia sekta binafsi ikakua mwisho wa siku ambapo karibia takribani asilimia 35 inaongeza kwenye GDP ya Taifa tunashindwa kuisimamia sekta binafsi.

Tunaomba sana Serikali isimamie hilo, na katika mpango huu tunaomba sana Serikali ihakikishe kwamba inaondoa vikwazo vizivyokuwa na maana katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ambayo kimsingi hayaendi sawasawa katika maeneo mbalimbali ya maendeleo. Tunazungumzia maendeleo ya watu, maendeleo ya watu hayawezi kukua bila kuwa na elimu bora. Leo hii wewe mwenyewe umezungumza hapo kwamba usajili wa watoto umeongezeka. Ni kweli Serikali imepeleka shule kwa ajili ya kujenga, lakini je, hizo trilioni zilizokwenda huko chini usimamizi wake ukoje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wabunge leo tumekuja ni moja ya sehemu ya fedha hizo, lakini usimamizi wake ukoje; tunahakikishaje kwamba hizo fedha zitafanya kazi kwa viwango na kutimiza ule wajibu ambao umekusudiwa? Kumbuka hili ni deni, wala siyo hisani kutoka kwa wale waliotupatia. Kwa hiyo, tunahitaji kuzisimamia, na Wabunge wenzangu naomba tuliangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya bado ninasisitiza kwamba tumekuwa na wimbo wa Taifa, kila siku tunarudia yaleyale lakini hayatimizi, tunapitisha kwenye bajeti ya Bunge lako Tukufu, mwisho wa siku fedha zinakwenda kidogo, tofauti na jinsi ambavyo tumeisimamia. Tunaomba kile tulichokipanga kama Wabunge kiweze kusimama kwenye Wizara husika na zikaenda kufanya kazi, hususan Wizara ya Kilimo ambayo ina asilimia kubwa ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusma hayo, ninaomba niishie hapa. Ahsante. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Mkataba wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika wa Kuzuia na Kupambana na Ugaidi ya Mwaka 2004
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana nami kupata nafasi ya kuchangia hoja iliyopo Mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja hii ilipita toka mwaka 2004 na nchi yetu ilisaini, lakini leo, miaka 18 baadaye, inaletwa Bungeni kwa ajili ya kuridhia. Ni hoja muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niwaambie Wabunge wenzangu, kama nchi, tunakosea sana tunaposaini mikataba mbalimbali ya Kimataifa, lakini ukifika wakati wa kuridhia na kupitisha Bungeni mnaleta kwa kuchelewa. Mmekosea sana, miaka 18 ni mingi sana. Mheshimiwa Waziri, kwa kweli umelichelewesha Taifa letu kuweza kusimamia nafasi hii ambayo leo tunataka tuifanye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi nimesikia Wabunge wenzangu wakiwaomba Wabunge waweze kuipitisha na kuiridhia. Ilitakiwa tuiridhie miaka 18 iliyopita. Hivyo basi, ninaamini leo, sote kwa umoja wetu, tutaipitisha ili tuweze kuisimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, itifaki hii ni ya muhimu, kama nilivyotangulia kusema, lakini nitaisema kwa upande wa pili. Sisi kama nchi tunapoenda kuiridhia, tunaomba tafadhali sana isimamie haki za binadamu. Kwa sababu itakapopitishwa, isichukue wale ambao ni watu wametuzidi kisiasa, wametuzidi kwa mambo mbalimbali ya kibinafsi wakati mwingine, kiongozi aliye madarakani au chama kilicho madarakani kikaamua kukandamiza watu kwa kupitia itifaki hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba itifaki hii itakapopitishwa, watu wafuatiliwe kiuhalali, wasimamiwe kama ni magaidi wafuatiliwe bila kuwabambikia. Kwa sababu tukiacha wazi watu wengi sana wasiokuwa na hatia wataweza kuhukumiwa, na baada ya miaka mitano, 10, 15, tunakuja kusema hawakuwa magaidi, tunawaachia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa njia hiyo hiyo kuna kipindi cha hapo nyuma watu wamefilisiwa mali zao, wamefungiwa akaunti zao za benki, wameshikiliwa pesa zao zisitumike mpaka uchunguzi uishe. Tunaomba itifaki hii ikasimamie haki za watu kama hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana, Ibara ya 18 ya Katiba inataka uhuru wa kujieleza, uhuru wa kutoa mawazo. Tunaomba itifaki hii isije ikawabana wale watu ambao wanatoa mawazo yao kwa ajili ya nchi yao, wakiwa wanatoa mawazo kwa ajili ya mambo mbalimbali yakiwemo ya kisiasa na ya kijamii, wasihukumiwe kama ni magaidi. Tunaomba ibara hii iwalinde na isimamie haki za hao watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinyume cha kufanya hayo, itifaki hii itaondoa amani na kuweka watu katika makundi, kwamba kuna watu wanaostahili kusema kitu fulani na kuna ambao hawastahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile hii itifaki pia iwashike wenzetu wa Jeshi la Polisi, waisome vizuri na kuiangalia. Kifungu cha tatu cha wajibu wa nchi washirika, kwa maana ya sisi ambao tunaingia itifaki hii, kipendele (a) kinasema hivi: “nchi mwanachama lazima ichukue hatua zote za kulinda haki za msingi za binadamu na kuhakikisha watu wake wanalindwa.” Watu wasipigwe, watu wasiumizwe wakiitwa magaidi wakati bado haijachunguzwa kama kweli hao watu ni magaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba ndugu zetu Polisi, maana yake wao watakuwa karibu sana na sheria hii na ndio watekelezaji kwa asilimia kubwa. Wasimhukumu mtu, hata kumtoa kwenye magazeti kama ni gaidi wakati bado hajathibitika kuwa gaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumzia habari za haki na umoja wa Watanzania. Tunaomba sana, itifaki ni ya muhimu, na ni vizuri kama walivyosema waliopita, nchi yetu inaingia kwenye uchumi wa kati, na kama inaingia kwenye uchumi wa kati, tunahitaji kuwa na amani na ulinzi, hata wawekezaji wanavyokuja kuwekeza wanajua tunakwenda sehemu salama. Mwisho wa siku tusiitumie vibaya tukafanya vibaya, hasa inagusa wanasiasa kwa sababu wanasiasa watakapoguswa, siasa ni hisia. Unapomkamata kiongozi wa kisiasa au mtu ambaye ameshindwana na ninyi kwenye mambo ya kisiasa mkamsingizia mambo ya ugaidi, amani itatoweka, watu hawatasimamia shughuli za kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba itifaki hii ipite. Nami nawaomba Wabunge wenzangu tuipitishe, lakini Serikali iliyopo madarakani ihakikishe itifaki hii inakwenda kusimama kwa haki kwa magaidi wa kweli na wala siyo magaidi wa kubambikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru nami kupata nafasi ya kutoa pongezi kwa ajili ya tuzo ya Rais aliyoipata. Sisi kama wanawake kutoka Beijing Platform tulikuwa tunatamani sana wanawake kuwa viongozi kwenye ngazi za juu za maamuzi. Mheshimiwa Rais kwa kupata nafasi hiyo, ninaamini anaitendea haki na ndiyo maana leo tunazungumzia habari ya kupata tuzo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikuwa tunasikia zamani Corazon Aquino kutoka Philippines kama Rais wa kule, tulikuwa tunasikia habari za akina Margaret Thatcher, lakini leo hii katika nchi yetu tuna Rais ambaye ni kiongozi. Vilevile leo tunapotoa pongezi hizi, kiongozi huyu amekuwa kiongozi wa 12 na inaonesha ni mwanamke wa kwanza kabisa kupata tuzo hii katika benki hiyo. Hii peke yake inamfanya yeye kuwa Balozi wa Afrika ili aweze kupata pesa za kuweza kujenga miundombinu tena Tanzania zaidi ya ile tuliyojenga, tuweze kupata maendeleo ya Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshauri Mheshimiwa Rais na kumpongeza kwamba yeye kama ni Balozi na amekuwa mwanamke wa kwanza kupata tuzo hiyo, basi nafahamu nchi za kwanza za dunia na za pili zitaona umuhimu wa kuleta fund katika nchi yetu ya Tanzania na kuweza kumsadia kumalizia majukumu yake hasa ya miundombinu ambayo bado kama Taifa tunahitaji kuijenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia kiongozi kupata nafasi, ni kusimamia kile ambacho watu wamekuamini wewe kukifanyia kazi. Nasi wanawake tuko vizuri sana kwenye maamuzi; tunapoamua kufanya kazi ya maamuzi tunasimamia kweli kweli. Mwanamke ana nguvu ya kuamua, mwanamke anapoamua kufanya kitu chake anaweza kufanya na akalisaidia Taifa kwa ajili ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe mwenyewe ni mwanamke, tunaona maamuzi unayofanya na kazi unavyoisimamia. Vivyo hivyo na sisi Wabunge wanawake tunapoamua; tukiamua, wako wanawake ambao hawaamui, lakini wanawake wanapoamua mambo yao, wakiona yana msingi kwa Taifa lao, wanasimamia wanachokiamini. (Makofi/Vigelegele)

MBUNGE FULANI: Haleluya! (Vigelegele/Makofi)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, niseme hivi; Mheshimiwa Rais, sisi kama wanawake unachokisimamia, kisimamie; simamia Watanzania, tuzo uliyoipata ni ya kwako, lakini ni ya Watanzania, hususan wanawake. Tunakuamini kwa kile unachokifanya lakini hiyo iwe ni chachu ya kusimamia mambo makubwa ambayo yako mbele kama Taifa na kama wanawake tunaenda kuyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, nampongeza kwa tuzo hii na atakapofika airport ninaamini wanawake watakuwa wa kwanza kwenda kuipokea tuzo hiyo maana ni ya kwao. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kutofuata Maelekezo ya Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami kuchangia ajenda ambayo Kamati imeleta. Kimsingi nami naiunga mkono.

Mheshimiwa Spika, kuna haja sasa baada ya haya kutokea, kuona umuhimu wa Mawaziri na Makatibu Wakuu kufanya wajibu wao kitaasisi. Nafikiri Mheshimiwa Waziri alipokwenda kuitambulisha ile timu aliyoichagua kwa bodi, kimsingi tu Katibu ilikuwa achukue jukumu la kuendelea kufanya shughuli za kiofisi na kuandika barua, ndivyo ninavyoona mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninalo swalli dogo tu kwamba, kwa nini hii bodi iliamua kuilipa fedha Kamati hiyo? Kwa sababu kama timu imechaguliwa kuja kukuchunguza, halafu unaenda kuilipa fedha, hakuna kitu ambacho kama unashawishi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najaribu tu kujiuliza kwa sauti labda kama sijaielewa Kamati. Kwa sababu wewe unaenda kuchunguzwa, halafu wewe bodi unatoa fedha kwenye hiyo timu; huoni kama kuna tatizo hapo? Kwa hiyo, hilo tu peke yake nilikuwa nalifikiria...(Makofi)

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Sophia Mwakagenda kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Neema Mwandabila.

T A A R I F A

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nilitaka nimpe taarifa dada yangu Mheshimiwa Sophia kwamba, nia ya Waziri ilikuwa ni kuboresha mfumo wa utoaji mikopo na siyo kufanya uchunguzi kwa bodi na ndiyo maana unakuta hata hadidu za rejea hizo mbili walizokuwa wamezitanguliza, wakajadiliana, na bodi ikashauri kwamba ziongezwe hadidu za rejea nyingine. Ingekuwa ni uchunguzi, nadhani bodi isingepata nafasi ya kuongeza hadidu za rejea kwa ajili ya hiyo kazi ya maboresho ya mfumo wa utoaji mikopo. Ahsante.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kimsingi najua Waziri amefanya kazi yake kama Waziri, na hapo mwanzo nimesema Makatibu na Wasaidizi wa Mawaziri kazi yao kubwa ni kuwasaidia Mawaziri kutimiza makusudi na kazi zao wanazozifanya. Nimesema bodi yenyewe ambayo inafanya kazi na Waziri, hatujasema imegombana na Waziri, lakini kama umepewa jukumu la kufanya kazi hiyo ya kuisaidia bodi kwa Watanzania na hasa wanafunzi wetu, kwa nini utoe fedha? Basi kama ni hivyo, basi kanuni zibadilishwe kama inawezekana. Mimi nafikiri hivyo, unless kama sijaielewa Kamati.

Mheshimiwa Spika, naomba, kukosea kupo, lakini hata kama wanasema amelidanganya Bunge, mimi sijaona kama amelidanganya Bunge, vinginevyo wewe usingetoa nafasi ya kufanya. Aliomba msaada wa kusaidiwa kuweza kuhakikisha Taifa letu linafanya kazi vizuri. Mimi sijaona kama ameshitaki, alifanya wajibu wake kama Waziri. Sijaona kama ni kitu kibaya, wala tusikichukulie hivyo, ndiyo maana wewe ukaona usimame kama mhimili kuhakikisha kazi hii inatendeka vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tupo hapa kwa ajili ya kujenga, kutengeneza na ndiyo maana sisi hapa tunaitwa Wapinzani, tunaotoa mawazo mbadala pale ambapo Serikali imekosea. (Makofi)

Kwa hiyo, ninaamini Mheshimiwa Waziri alikuwa sahihi, bodi iko sahihi na kuanzia sasa bodi itakuwa very sensitive, kwa sababu tayari imeshaona kumbe ukikosea kidogo unaweza ukaitwa, unaweza ukaenda kufanywa kitu fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaunga mkono hoja ya Kamati, naipongeza na maoni yao yazingatiwe, na Wabunge wenzangu tuyawekee mfumo mzuri na tuyakubali maoni yao. Ninampongeza Waziri na ninaipogeza bodi vile vile maana tunataka kusonga mbele, hatutaki kurudi nyuma. Ahsante. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Wakala wa Kimataifa wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu (International Renewable Energy Agency - IRENA) na Azimio la Bunge kuhusu mapendekezo ya kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika wa Mwaka 2019 (Treaty for the Establishment of the African Medicine Agency - AMA)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia eneo hili. Wenzangu wamekwishakueleza kwamba kitu hiki kilianzishwa tangu 2009 mpaka 2011 ndipo ilipoanza kazi. Lengo kuu kabisa na malengo manne kutokana na Wizara walivyoweza kutueleza lakini mimi tataja malengo makubwa mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhamasisha teknolojia mbalimbali za kusaidia kuweza kupata nishati salama; la pili ni kuwezesha upatikanaji wa nishati safi na salama yenye gharama nafuu, tunajua kabisa fika kama Taifa kutegemea umeme huo mwingine ambao tunaotegemea sasa tunapitia kwenye madhira makubwa sana kutokana na tabianchi pia. Hivyo tutakapoamua kupitisha itatusaidia sana kuweza kupata umeme huu mwingine ambao tunafikiri utakuwa mzuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, jukumu kubwa sana sana la hii IRENA ni kujengea uwezo nchi mwanachama. Tunajua watalamu wetu watajengewa uwezo, lakini pamoja na hayo kwa jinsi ambavyo tumeelezwa na tumesoma tumeelewa tutakapojiunga kuwa wanachama ni rahisi kupata fedha kwa ajili ya kusaidia Taifa letu na kuweza kusaidia teknoloji hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, itatusaidia sana pia kupata umeme kwa urahisi zaidi ikiwemo gesi joto ambazo tayari utafiti umekwishafanywa. Na ili uweze kufanikiwa Serikali imeamua kuanza kufanya utafiti na kuweza kuelewa ni maeneo gani ambayo tunaweza tukapata nishati hii. Hilo peke yake hata wawekezaji itakuwa ni rahisi kufika kwa sababu tayari tumekwisha warahisishia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niseme kama Mjumbe wa Kamati lakini kama Mbunge mwenzenu kwamba kuna haja ya kupitisha sheria hii. Mimi siilaumu sana kwa kuchelewa kwa sababu wasi wasi ni akili. Mimi naamini muda mrefu uliyochukuliwa imetusaidia sisi kujua kwa kina, watalamu wetu kusimamia kwa kina. Kwa hiyo tusikimbie kusema tungefanya haraka hivyo walivyochelewa wamefanya vizuri na sasa ndiyo wakati sahihi wa kutoa maamuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze Wizara mnaendelea; na kuna maeneo mengine tufanye taratibu kama nchi tukubaliane mwisho wa siku tupitishe kwa umoja. Ninaipongeza Wizara, ninampongeza Waziri husika kwa kuwa amefanya vizuri, pia hata Katibu wa Wizara amefanya kitu kizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninaamini baada ya kupitisha IRENA tutaenda kufanikiwa kama Taifa. Wameishasema wenzangu kuna nchi ambazo zimetutangulia katika East Africa, tunafahamu Uganda na Kenya pamoja na Rwanda walishajiunga. Kwa hiyo na sisi tutakapojiunga Taifa letu linaenda kupata faida na kwa hivyo ninaunga mkono kwa mara ya kwanza mia kwa mia tuunge ajenda hii, ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuchangia Mpango huu wa Mwaka Mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie habari ya tozo ambazo huwa tunatozwa kwenye miradi mbalimbali ya Serikali inayofanywa. Binafsi ninasikitika sana kwa sababu pesa ambazo Wakandarasi wakubwa wa nje na Wakandarasi wa ndani ambao wanakuja kudai Serikali ni pesa nyingi sana. Mpaka sasa zaidi ya Bilioni 12 tumelipa kama Serikali kwa ajili ya faini mbalimbali ambazo hawa Wakandarasi wameipiga Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwamba Mheshimiwa Waziri, tunapoweka mikataba yetu naamini tunao wanasheria mahiri sana katika Taifa hili ambao wamesomeshwa kwa kodi za wananchi inakuwaje wanachelewesha kuwalipa na kupelekea Taifa Kwenda kulipa pesa nyingi kiasi hiki kwa ajili ya kulipa faini ambazo zinaendelea. Inabidi iundwe Tume maalum ya kuangalia tatizo hili, inawezekana kuna watu wanafanya maksudi na wanafanya hizo deal ili waweze kula hela za Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siamini kwamba tunajua tunahitaji kuendelea kulipana kwa wakati halafu Maafisa Masuuli hawawalipi Wakandarasi hawa mwisho wa siku deni lile linaenda kwa mwananchi wa kawaida ambae ndiye mlipa kodi ambaye pesa yake hii Bilioni 12 ilikuwa na uwezo wa kwenda kuongezea madarasa haya ambayo yanajengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini ninasema kitu hiki ni kibaya? Miradi inapocheleweshwa na tunakwenda kulipa faini, kwanza inaondoa value for money, miradi ile pia inakuwa haiendi kwa wakati, lakini pia inakuwa chini ya kiwango kwa sababu usimamizi unakuwa si mzuri. Kama mradi ulitakiwa kwisha mwaka huu unapomalizia mwakani hata ufuatiliaji wake, ile monitoring and evaluation haiendi sawa. Mimi ninafikiri sasa ni wakati kama Taifa tuhakikishe maafisa masuuli na wanaohusika kuchelewesha watu kulipwa wachukuliwe hatua kali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ifike hatua sasa Serikali ilete muswada hapa Bungeni ili kupitia Muswada huu itungwe sheria ambayo itafanya yeyote anayechelewesha achukuliwe hatua ili tuweze kusonga mbele kama taifa; na fedha nyingi sana ambazo zinapotea ziweze kurudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mifano ya miradi ambayo tumewalipa hela nyingi sana. Kigongo – Busisi kwa mujibu wa CAG ripoti yake ya mwezi Machi, ukurasa wa 185 anasema tulichelewesha kuwalipa na wao wakatupiga fine ya bilioni 1.5 hizi fedha ni nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ripoti ya CAG huyohuyo kuhusiana na SGR anasema tulipochelewa kuwalipa wale wakandarasi tumeweza kuwalipa kama Taifa pesa zaidi ya bilioni 3.144. Hizi fedha ni nyingi sana kwa Watanzania, zingeweza kusaidia kwanye bajeti ya nchi na tukaendelea na maendeleo kama kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie miradi ya barabara. Kumekuwa na ahadi nyingi sana za barabara. Tunaambiwa tumetoa fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu. Tumetolewa fedha, kwa mfano kuna barabara inayokwenda Soni – Bumbuli mpaka Korogwe kilometa 74. Hii ilitolewa fedha takribani milioni 924 kwa ajili ya upembuzi yakinifu, lakini ukifika wakati wa bajeti nyingine inakuta bado tuko palepale hatujaanza kuufanyia mradi ule kazi, zile fedha zinakuwa zimelala. Na hiki inawezekana ni kichochoro cha watu kupitishia fedha za kuweza kuliibia Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya Mtwara – Newala na Masasi kilometa 221; zimepelekwa fedha za upembuzi yakinifu wakati huohuo inatengwa bajeti na mwaka mwingine ukija bajeti bado iko palepale. Tunaomba ufuatiliaji wa miradi kama huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie mfumuko wa bei. Tunapozungumzia mfumuko wa bei kiukweli unamzidishia mwananchi wa kawaida maisha kuwa magumu; chakula na mahitaji ya muhimu ya kimsingi bei imekuwa juu sana. Kama Taifa na Mheshimiwa mwenye Wizara husika tunaomba tumsaidie mwananchi wa kawaida ambaye kimsingi mfumuko wa bei kwa sasa umepanda umekuwa asilimia 7.8 ilhali inahitajika tusivuke asilimia tatu kama Taifa. Mfumuko wa bei unapokuwa juu maisha yanapanda. Tunaomba tusimamie tuhakikishe tunakuwa tuko sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya ninaunga hoja, lakini tuhakikishe tunasimamia yale ambayo tumekubaliana kama Taifa. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi kupata nafasi ya kuweza kuchangia mada zilizoko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, ninapenda tu kuiuliza Serikali kwa wenzetu wa TANROADS. TANROADS katika bajeti ambayo tuliipitisha katika Bunge lako Tukufu ni asilimia 24 tu peke yake zimeweza kutoka kwa ajili ya kufanya kazi, katika asilimia hizo 24, asilimia 7.2 ndiyo zimejenga madaraja, kwa hiyo barabara nyingi sana katika Taifa hili zinachelewa sana kujengwa.

Mheshimiwa Spika, barabara ndiyo maendeleo, wewe unaona wakati wajumbe hapa wakiuliza maswali ya barabara zao kwenye Majimbo. Usipokuwa na barabara imara na usipokuwa na barabara wakulima hawawezi kufanya chochote kwa sababu bidhaa zinapanda, barabara hazifikiki na wale wakulima hawafikiwi mapema. Ninapenda kujua kwa Serikali na hasa Wizara ya Fedha, kwa nini fedha haziendi kwa wakati ili kuweza kuwasaidia hawa watu?

Mheshimiwa Spika, nilijaribu kuuliza wakasema kipindi cha manunuzi labda kinachukua muda mrefu, labda ifike wakati hata Sheria ya Manunuzi iweze kubadilika, kwa sababu kuna baadhi ya miradi inachelewa kwa sababu zile Sheria zinamlolongo mkubwa sana, kama ikibidi basi Serikali ilete ile sheria upya turekebishe ili mambo yaweze kwenda kwa kasi kama tunavyotaka ili mambo yaende. Barabara ni kilio kikubwa sana kwa Wabunge kwenye majimbo yetu, barabara hazipitiki, barabara zimekuwa zinachukua muda mrefu sana kwa usanifu, mchakato na lugha kama hizo, tunahitaji kubadilika.

Mheshimiwa Spika, misamaha ya kodi kwa TANROADS. TANROADS inapotaka kufanya kazi, misamaha kwenye Wizara ya Fedha inachelewa kutoka na hii inapelekea wasiweze kufanya kazi kwa haraka. Kwa hiyo, tunaomba Serikali isimamie hilo ili tuweze kuwasaidia ndugu zetu. Kwa upande wa TANROADS hao hao, naomba utaratibu wa kupima mabasi kwenye mizani nafikiri nia ilikuwa njema hapo zamani, lakini sasa hivi basi linajulikana linabeba abiria kiasi gani, basi likishapima mwanzo likapime na mwisho hapa katikati wasipime kwa sababu inaongeza msongamano na foleni kwenye barabara. Kuna wakati mabasi yanakaa masaa mawili hadi matatu yakisubiri kupimwa, mimi nafikiri uchumi ni muda, unapopoteza muda uchumi pia unapotea. Kwa hiyo, ninashauri ikiwezekana wenzetu wa TANROADS waruhusu mabasi yapimwe mwanzo wa barabara na mwisho wa barabara hapa katikati kama wanafikiri wanaongeza mizigo kwa magari mengine ni sahihi lakini kwa mabasi nafikiri abiria wanapata shida sana, kwa hali hizi za kupima mizani inachukua saa nzima masaa mawili watu wako kwenye foleni.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la TCRA, kumekuwa na shida kubwa sana ya utapeli kwenye simu. Message zinazoingia kwenye simu bila mteja kukubali kupokea message. Kwa mfano, mganga maarufu kutoka sehemu fulani, wanapata wapi hizo namba, wanafanyaje? Kwa hiyo, tunaomba TCRA itusaidie. Siyo hivyo tu, wanatuma meseji ninaamini Viongozi hapa tunapata message wanasema kuna shida kuna kitu fulani nitumie, ukituma tuma kwenye namba hii na usipojitambua labda mwenyekodi alikudai ukajichanganya ukatuma hela imeondoka. Tunaomba watusaidie TCRA na hasa Serikali ikiwawezesha TCRA kuweza kusimamia majukumu yao na kuhakikisha wanazuia huu wizi wa mitandao ambao umekuwa ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ninafahamu Waziri anaehusika amesimamia vizuri hili kuhusu uzimaji wa laini. Zipo laini nyingi sana ambazo zimesajiliwa, zingine zimesajiliwa kwa njia ambazo jina la Mwakagenda lipo lakini siyo laini ya kwangu, amesema vizuri Mheshimiwa Waziri tunataka zizimwe na kweli zizimwe ili tuweze kujua walio genuine ni nani na ambao siyo genuine ni nani. Kwa hiyo, mimi naunga mkono suala la kuzima laini na hasa wale ambao hawajahakiki mjitahidi mhakiki ili msiweze kuzimiwa laini zenu.

Mheshimiwa Spika, ninaipongeza TBC kwa maana ya kwamba imejenga Studio mpya pale Dar es Salaam lakini na Dodoma pia na imeweza kufanya vizuri, tumewekeza pesa nyingi sana zaidi ya Bilioni Kumi, mwisho wa siku usipowekeza kwa wafanyakazi, unakuwa hujafanya lolote. Kwa hiyo, Wizara hii ihakikishe, pamoja na kutengeneza Studio zetu vizuri ikiwepo Radio Tanzania ile ya zamani wamei-modify imekuwa nzuri lakini wafanyakazi walipwe posho wanapokwenda kwenye kazi zao, kwa sababu wao ndiyo wanaolisaidia Taifa hili. Mheshimiwa Rais akienda mahali wanaenda, walipwe posho kwa wakati ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tupo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, tunaangalia channel za wengine, wafanyakazi wanavaa nguo nzuri kwa kudhaminiwa na maduka pamoja na makampuni. TBC inahitaji kufanya kitu kama hicho ili wafanyakazi wetu waonekane na mwonekano mzuri na waweze kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia usikivu mipakani kumekuwa na shida, huko bado kunahitaji kuongeza fedha kwa ajili ya kutengeneza mitambo tuweze kusikia habari za huku kwetu. Ukienda Tunduma, Kyela, Kyerwa na sehemu zingine kama Kigoma unakutana na redio za nje ya nchi ambazo ziko kwenye hizo sehemu. Unakuta redio Malawi inasikika Kyela, kwa hiyo tunaomba usikivu uweze kuongezeka. Pia wanahitaji OB Van, tunaamini Serikali itaongeza fedha kuhakikisha mitambo ya TBC inakuwa mizuri.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo nizungumzie kuhusu TBA. TBA ilipoanzishwa Sheria yao ilikuwa inataka kuhudumia tu mambo ya kiserikali na nyumba za kiserikali, sasa hivi tunaingia kwenye utandawazi, tulete Sheria Bungeni ili TBA waweze kufanya biashara, kwa sababu kama real estate kama watu binafsi wanatajirika, hata hawa watu tukiwawezesha wanaweza kufanya kazi vizuri sana. Kwa hiyo, naomba sheria iletwe ili TBA ibadilike na hawa watu waweze kukopa na siyo tu kukopa waweze kushirikiana na mashirika mengine wakaweza kujenga na kuisaidia Serikali kupata nyumba nyingi sana na zaidi ya yote tuweze kuhakikisha hata Wabunge wanaohitaji nyumba kama Dodoma waweze kupata kwa sababu hawa TBA wanahitaji fedha ili waweze kufanya haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, ninaunga mkono hoja za Kamati na mapendekezo ya Kamati ambayo wameyatoa katika Bunge lako, tunaamini Serikali itayafanyia kazi. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii. Kama walivyosema wenzangu waliotangulia bado nampongeza Mheshimiwa Waziri Bashe, kwa kuwa amekuwa mwepesi, tunapompelekea matatizo yetu kutusaidia hususani sisi watu wa Nyanda za Juu Kusini ambapo ndiyo tunalima sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imezungumza habari ya pembejeo na hasa tukienda kwenye eneo la mbolea; kwa muda mrefu imekuwa bei pamoja na kwamba wameizungumzia, wananchi wamepata shida sana, sana katika ulimaji msimu huu wa kilimo. Tunafahamu kabisa na Mheshimiwa Waziri amesema kwamba dunia imepandisha bei, lakini mwisho wa siku Watanzania wana Serikali yao ambayo wanaitegemea na tunajua kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo kama ambavyo tulikuwa tukisema miaka mingi, watanzania hao wanahitaji chakula. Sasa Serikali kuchelewa kutoa maamuzi ya kuwasaidia wakulima na hasa kuweka ruzuku kwenye mbolea, nafikiri wamefanya kosa kubwa sana la kutufanya tusiwe na chakula kipindi kinachokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia mbolea kupanda bei, DAP ilikuwa shilingi 66,000; Urea ilikuwa Sh.53,000, mbolea hizi zilifika mpaka bei ya shilingi 150,000 kwa mfuko wa kilo 50. Sasa kuna haja ya Mheshimiwa Waziri kuona matatizo yanapotokea kuwa na first truck ya kuamua kuweza kusaidia Watanzania. Kwa kukaa kimya mpaka leo bajeti imekuja na Waziri anatamka na hatujui utekelezaji wake utachukua muda gani, kwa kweli hatujawatendea haki wakulima wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amezungumza kwenye hotuba na naweza kumwamini kwa sababu naamini anaweza kufanya kazi...

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti naomba kumpa mzungumzaji taarifa kwamba, pamoja na kwamba mbolea ilikuwa bei ya juu, lakini bado upatikanaji wake ulikuwa ni changamoto kwa wakulima wetu. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwakagenda unaipokea taarifa?

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea. Tunaamini kwa uchapa kazi wa Mheshimiwa Bashe, bajeti hii ameipata moja kwa moja akiwa Waziri, kwa hiyo, alichokisema hapo kwamba anaenda kuhakikisha mbolea inashuka bei, lakini si tu, hivyo inapatikana kwa wakati ili wakulima wasiingie kwenye matatizo. Tunaomba Mheshimiwa Waziri alitekeleze hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la chai. Zao la chai ni zao kubwa sana katika nchi yetu ya Tanzania. Mikoa inayolima chai au sehemu zinazolima chai, Lushoto, ukienda Muheza, Njombe na Rungwe kwetu tunalima sana chai. Nimekuwa nikisema mara nyingi hapa Bungeni na nikiongea na Mheshimiwa Bashe juu ya zao hili. Zao hili kwa ripoti ya Bodi ya Chai yenyewe, inasema uzalishaji wa chai umepungua kwa asilimia nne katika mwaka uliopita. Kwa nini zao hili linapungua kwa wakulima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao hii linapungua kwa sababu bei yake haipandi na bahati mbaya sana Bodi ya Chai kama wapo hapa wananisikiliza wanapendelea maeneo kwa maeneo. Nchi ni moja lakini chai inauzwa bei tofauti tofauti. Ukienda Rungwe chai haizidi Sh.230, lakini ukienda Njombe unakuta chai kilo moja ni Sh.500. Nchi moja, wakulima hao hao, Rais wao mmoja, lakini bado tumewagawa kwenye bei. Sijaelewa ni vigezo gani Bodi ya Chai inatumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, Bodi ya Chai haisimamii haki ya wakulima, kuna makampuni yanayonunua chai mbichi, lakini wakulima kwa muda mrefu hawalipwi madeni yao bila sababu yoyote. Sisi tunaamini Bodi ya Chai ndiyo msimamizi wa wakulima wasiokuwa na sauti, lakini bodi hii imeungana na wanunuzi, imeungana na makampuni na kuwaacha wakulima wakihangaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la pembejeo kwa wakulima wa chai. Makampuni haya yanatoa mikopo ya mbolea kwa bei ambayo si nzuri. Mtu anapewa mfuko wa mbolea kwa bei iliyo juu, akija kuuza chai anakuja kukatwa, mwisho wa siku mkulima anabaki na fedha ndogo sana. Naomba Mheshimiwa Waziri alisimamie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii chai nimeizungumzia muda mrefu na naomba sana, sana kwa maelezo ya CAG, ukaguzi uliofanyika mwaka huu Machi, 2022, makampuni sitaki kuyataja hapa, yamekopa wakulima toka 2018 mpaka leo hii hawajawalipa madeni yao. Naamini Mheshimiwa Bashe anayamudu makampuni haya, naomba ayasimamie ili wawalipe wakulima stahiki zao, kwa sababu wamefanya kazi kwa jasho na sasa wanahitaji kutumia fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Benki ya Kilimo; benki hii ipo kwa ajili ya wakulima, lakini kwa mfano, kwa wakulima wadogo wadogo, kuna mfuko ambao ulitolewa pesa zaidi ya bilioni 7.0 kwa ajili ya kuwakopesha wakulima wadogo wadogo, lakini pesa hii kwa mujibu wa CAG kwenye ripoti ya Machi, 2022, walichukua pesa hiyo wakabadilisha matumizi badala ya kuwakopesha wakulima wadogo wadogo. Pesa hiyo ikaenda kufanya kazi nyingine bila kuwasaidia hao wanaohitaji msaada wa kukopa. Naomba hilo pia Mheshimiwa Waziri akija kuhitimisha anipe maelezo tuweze kuelewa ilikuwaje, kwa sababu mwisho wa siku wakulima wakubwa wanafaidika na walio wengi ambao ni wadogo hawapati chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba Benki ya Kilimo lengo lake ni kusaidia Watanzania, tunaomba isimamie lile kusudio ambalo imepewa na Serikali. Pia kuna Mfuko wa Pembejeo, Mfuko huu unaenda kufilisika kwa sababu zaidi ya bilioni 27 ambazo zilitolewa, bilioni 20 zimekopwa na hazijarudi. Sasa tunawezaje kusaidia Watanzania kama kuna fedha zinatolewa halafu hazirudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Mheshimiwa Waziri ametoa kwenye hotuba yake akisema, anataka watu wanaouza pembejeo mbolea waungane. Naamini katika mipango mizuri aliyonayo Mheshimiwa Waziri au iliyonayo Serikali yake, lakini mwisho wa siku utekelezaji haupo. Kupanga ni kitu kingine na kutekeleza ni kitu kingine. Kwa hiyo, Mfuko huu zaidi ya asilimia 72 pesa bado ziko mikononi mwa watu, hazijarudi wakati sisi tunategemea pesa hizi ziweze kusaidia wale wengine ambao bado hawajakopa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalima parachichi kama alivyosema Mheshimiwa Waziri na watu wamejitokeza kulima parachichi kweli kweli, lakini kwenye export ya parachichi tunashindwa kujenga kiwanda cha kutengeneza box la kuhifadhia parachichi mpaka twende Kenya tukanunue. Nafikiri hatujitendei haki kama Watanzania kwa sababu kujenga kiwanda cha kutengeneza box hapa, tutatoa ajira kwa vijana na tutapunguza gharama ya ku-export parachichi, badala ya kwenda kuagiza Kenya, order inachukua mpaka siku nne mpaka siku saba, mtu aipate kutoka Kenya, ije Rungwe iende Makete, tunakuwa hatuwatendei haki Wtanzania. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii. Kabla ya yote ninakualika kwenye pambano la ngumi tarehe 23 jumapili kwa ajili ya kuchangia taulo za kike wewe pamoja na Bunge lako; lakini ninajua majukumu yako ni mengi, nilitamani sana uingie ulingoni nimekuandalia Mwasi Kamani upambane naye kama utapata nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niendelee na kuchangia.

Mheshimiwa Spika, katika Wizara hii nitazungumzia leo walimu peke yake. Mheshimiwa Waziri katika Wizara yako kuna shida kubwa sana ya kupandisha madaraja kwa walimu. Walimu wanfundisha kwa moyo wakati mwingine ameenda kuongeza elimu kwa ajili ya kuweza kufanya kazi zao kwa ufanisi, lakini upandaji wa madaraja umekuwa ni shida na Serikali mliamu akila baada ya miaka mitatu angalau mwalimu akijaza zile fomu za OPRAS aweze kuongezwa daraja. Hata hivyo, na wale waliobahatika kuongezwa madaraja hawalipwi stahiki zao kwa wakati; hiyo si kabisa, tunavunja mioyo ya walimu kwasababu wanashindwa kufanya kazi na kufundisha watoto wetu.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana bajeti iliyopita walisema wataweka kitu kinachooitwa mserereko, kwa maana ya kupandisha daraja kwa haraka haraka kwa kuwa kwa muda mrefu hayajapandishwa. Ndugu zetu mmejisahau, ninaomba bajeti hii muwakumbuke watu wapandishwe madaraja lakini.

Mheshimiwa Spika, walimu wanaoajiriwa ajira mpya wanacheleweshewa mishahara mpaka miezi mitatu, hii pia inaongeza kuwafanya wafanye chini ya kiwango kwa sababu usipokuwa na mshahara unacheleweshwa inakuwa ngumu zaidi. Wakati mwingine hata arrears zao ambazo zinatakiwa walipwe mnaanzia pale walipoanzia. Mheshimiwa Waziri mimi nakufahamu wewe ni gender activist hakikisha unatetea watu hawa wafanye kazi sawasawa.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia capitation kwa sasa mnafanya vizuri, ninaamini, lakini kuna baadhi ya walimu wakuu hawana fedha hivyo wanaamua kuanzisha miradi midogomidogo ndani ya shule. Nikizungumzia miradi namaanisha uanzishwaji wa kambi za kujisomea wanafunzi. Mimi ninakubali, na hasa Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa Mtaka alipoanzisha ilikuwa na tija kidogo; lakini kuna wengine wanafanya kama biashara. Wanawaweka watoto kwenye kambi na kulazimisha wachangie fedha nyingi, ambazo sasa tunarudi kule kule kuwapa mzigo wazazi. Tunataka ubunifu wa uhakika lakini usiwe ubunifu unaombana mzazi au mtoto ashindwe kwenda kwenye hilo darasa la jioni la kujiendeleza kwa ajili ya kufaulu.

Mheshimiwa Spika, mimi ninaamini sana katika mambo ya ushindani na hasa ushindsni wa tija usio ushindani wa kuharibu. Vyama vya Walimu (CWT) na vyama vingine; kuna chama kipya kinaitwa CHAKAMWATA na vinginevyo mviache viwe huru ili walimu waweze kutoa hoja zao, waweze kulalamika kwa uhalali na hatimaye zile changamoto walizonazo katika maeneo ya kazi ziweze kujibiwa. Tunapozuia vyama vya wafanyakazi na kuwawekea viongozi na kuwalazimisha hatuwatendei haki walimu. Tunataka wao wachague wanao wataka na hatimaye waweze kujikwamua katika tija wanazotaka kufanya.

Mheshimiwa Spika, naomba sana; suala la walimu wa kike amelizungumza mbunge aliyeondoka; tusipokuwa na walimu wa kike ilhali sasa hivi tunajua dunia imeharibika; hali inakuwa mbaya katika malezi ya watoto wa kike. Tunahitaji walimu wawepo ili waweze kuwasimamia watoto hawa na hatimaye watoto waweze kufanikiwa.

MHE. JOSEH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Sophia Mwakagenda kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa George Kakunda.

TAARIFA

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji. Zipo shule nyingi jimboni kwangu hazina mwalimu wa kike kwa hiyo watoto wa kike wanakosa huduma ya kuhudumiwa na mwalimu wa kike.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge niwakumbushe tu taarifa inatumia muda wa mchangiaji si muda wa kiti. Mheshimiwa Sophia Mwakagenda malizia.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante ninaipokea taarifa hiyo na ninasisitiza kwamba mtoto wa kike anapohudumiwa na mwalimu wa kiume ndipo ubakaji na mambo mabaya yanaanzia hapo. Kwa hiyo, tunaomba Wizara hii ihakikishe kuwa katika bajeti hii tunaajiri wanawake kwa wingi zaidi kwa ajili ya watoto wa kike kwenye shule zetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya ninakushukuru sana kwa kunipa muda wa kuchangia na ninaendelea kukuombea ukubali kupambana na Ng’wasi kama utakubali, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimkumbushe Mheshimiwa Waziri kwamba mwaka jana tumefanya sensa ya Taifa na wenzetu wa NBS wametoa takwimu nzuri kabisa juu ya mifugo tuliyonanyo katika Taifa letu. Ng’ombe tunao zaidi ya milioni 35, mbuzi milioni 25.6 na wanasema kondoo tunao takribani milioni nane. Hii pee itakusaidia wewe kupanga mipango yako vizuri kama wizara na kuhakikisha tunasaidia Watanzania kuvuka kwa mahitaji ya mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao ya ng’ombe na wanyama yameliingizia Taifa hili dola takribani milioni tatu. Hii ni hela ambayo kimsingi ikiongezewa nguvu tutapata zaidi ya hiyo pesa, kuweza kusaidia uchumi wa Taifa letu. Tatizo kubwa lililopo katika Taifa hili ni mipango na utekelezaji. Waheshimiwa Wabunge wenzangu wengi wameelezea suala hili. Huwezi kuwa na mipango ambayo unaingiza nyama na wakati huo huo una wafugaji wako, na hawa wafugaji hujawajengea uwezo wa kulisha. Wamesema hapa, ng’ombe miaka minne ana kilo 80 wakati wenzetu ana zaidi ya kilo 500. Ni lazima tufanye kazi ya kuwasaidia Watanzania waweze kutoa bidhaa bora kuweza kusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaambiwa Tanzania ni nchi ya pili kati ya nchi zenye mifugo mingi. Kwa nini sisi tusizalishe zaidi ya wenzetu ambao wanafanya vizuri, kama vile Botswana na nchi zingine? Mimi ninafikiri Waziri wa Fedha anahusika zaidi kutoa fedha kwenye Wizara hii. Nilikuwa nikiongea na Naibu Waziri anasema tukipata fedha tuna uwezo wa kufanya maajabu katika wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakaa hapa kama Bunge tukipanga mipango mingi lakini kutoa fedha hatuwezi kuwasaidia. Wataalam tunawalaumu, kwamba wapo, wamesoma na wapo ofisini wanalipwa mishahara, lakini usipowapa fedha hawawezi kufanya yale ambayo tumewapa, mwisho wa siku bajeti inakuwa ndogo. Tunakubaliana hapa kama Wabunge mwisho wa mwaka wanafanya fedha asilimia mbili, asilimia tatu; hatujafahamu ni nini mnakifikiria ilhali mnajua kabisa wizara hii ina wakulima na wafugaji wengi. Hao ndio wanaoweza kuongeza Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ukosefu wa miundombinu, lakini pia miundombinu si salama na si rafiki kwa ajili ya wafugaji. Tunazungumzia maziwa kwa mfano, jana tumepata maziwa hapa kama Wabunge, lakini bado mfugaji amekuwa mtumwa wa ng’ombe au wa mifugo yake. Kwa mfano kule kwetu Rungwe lita moja ya maziwa ni shilingi 600; leo hii maji yana thamani kubwa kuliko maziwa. Mfugaji analala na ng’ombe anaamkia ng’ombe, akifiwa anamuwaza ng’ombe kwanza kuliko ndugu yake aliyefariki lakini mwisho wa siku lita moja shilingi 600; hatuwatendei haki wakulima. Tunaomba bei ya maziwa iongezeke. Maziwa ni chakula, huwezi kuuza maziwa lita moja kwa 600, maji madogo ya chupa nusu lita shilingi 1,000, hii si sawa kabisa. Inabidi kujipanga viongozo ili tuhakikishe tunawatetea wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa masoko, tulikuwa na kombe la dunia, tulipatapata kidogo masoko ya nyama, lakini mwisho wa siku, wamesema Waheshimiwa Wabunge waliopita; thamani ya nyama yetu miundombinu inayotengenezewa inafanya sisi tusipate soko la dunia kwa vizuri zaidi. Amesema hapa Mheshimiwa Mhagama, kwamba anayetoa nyama kutoka Afrika kuipeleka Dubai ni karibu zaidi kuliko anayetoka Brazil kuileta pale Dubai. Inabidi tukae chini na tujitafakari ili tuone nanma gani tunafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mlipuko wa magonjwa wananchi wenyewe wanaamua kujitetea. Magonjwa ya mifugo yanapokuja wao wenyewe wanaamua kuona namna gani wanadhibiti. Tunaomba Serikali isimamie. Maafisa Ugani ni wachache mwisho wa siku wananchi wenyewe wanaamua kujisimamia badala ya ninyi kufanya kama Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uwekezaji mdogo, nimesema kuna viwanda vya uwekezaji, tuna machinjio ambayo kiukweli mengi; unajua nchi za kiarabu ndio wananunua zaidi nyama. Kwa hiyo ni lazima tuwahakikishie wenzetu waarabu ambao wao wanapenda nyama halali, kwa hiyo tuwahakikishie kwamba nyama yetu ni salama ili wawe huru kuja kununua nyama kutoka kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna nguvu zaidi inabidi kuongezeka. Tuna tani zaidi ya laki saba za nyama ambazo zinavunwa, lakini kwa jinsi tulivyo tunahitaji kupata nyama zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wafugaji na ufugaji wa kuhamahama. Ninajua wenzangu ambao wanatoka maeneo ya wafugaji watalalamika, lakini tufike mwisho, tupande majani kwa ajili ya wanyama wetu waweze kula katika maeneo yetu kuhamahama kupungue ili tuweze kupata nyama iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumzia suala herein, nashukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu jana ametolea maagizo kwa Mheshimiwa Waziri; tunaomba alifanyie kazi haraka, kwa sababu tunatoa matamko; leo anapigwa chapa kesho mnasema herein, lakini mwisho wa siku utekelezaji unachelewa. Ninaomba sana uyasimamie aliyoyasema Mheshimiwa Waziri Mkuu jana ili yaweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo tunaomba Waziri wa Fedha pamoja na Serikali ya Chama cha Mapinduzi ongezeni fedha kwenye wizara hii, ili Watanzania waweze kunufaika na Wizara yao. Baada ya kusema hayo nasema ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kupata nafasi na mimi kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, ninampongeza Waziri kama wenzangu walivyosema, pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo wameweza kuchangamsha Idara na Wizara ya wanawake kuonekana sasa tupo na tunaweza tukapiga kelele kwa sauti kubwa.

Mheshimiwa Spika, bado tuna changamoto nyingi sana, leo nitazungumza chache nikianza na suala la mauaji kwa kutumia mapenzi. Tumeona kwa siku za hivi karibuni kumekuwa kuna mauaji makubwa sana kisa wivu wa mapeni. Mheshimiwa Waziri, kuna haja kubwa sana sasa ya kupiga kelele. Na suala hili haliko Tanzania peke yake, watafiti wa haki za binadamu wamefanya utafiti, mwaka 2021 na 2022 kwa dunia nzima takribani wanawake 45,000 wamekufa kwa wivu wa mapenzi, kwa Afrika Mashariki peke yake, asilimia 43 wanawake wanapigwa, wasichana wanapigwa na vijana kisa wivu wa mapenzi, na wakati mwingine hawana uhakika, ni wivu tu umewatokea anaamua kutoa roho ya mtu kwa sababu ya kumuonea wivu. Mheshimiwa Waziri, kuna haja ya kupiga kelele katika eneo hili.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanafunzi wa vyuo, wanandoa, wanapigana wanauana na kuacha watoto mitaani wakizunguka kisa tu baba aliona simu au mama aliangalia simu ya mumewe na kuingia kwenye matatzizo. Labda niseme tu hili pia kwamba tuna haja sasa ya kujijenga tabia njema katika familia kwa sababu mwisho wa siku wivu umeondoa roho za wanawake wengi katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, ukatili wa kisaikolojia. Kuna Mbunge mwingine amezungumza hapa, leo hii takribani ndoa zaidi ya 700 zimeripotiwa katika kuwaumiza wanawake kwa kuwaacha. Mwanaume anamwacha mwanamke na watoto watano, watoto 10 anakwenda kuoa nyumba ndogo na kumwacha mke wake na kusababisha yule mwanamke kupata msongo wa mawazo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, kuna namna nafikiri watu wanaohusika na afya za akili na ustawi wa wanawake wanasimamia suala hili. Kwa sababu Mheshimiwa Waziri, leo hii tunataka kujenga Taifa la kesho, unalijengaje Taifa ambalo mtoto anaona mama yake anapigwa mbele yake? Mtoto anaona baba mtu anaingia usiku na matusi kwa sababu tu kalewa anatamka maneno yasiyofaa katika familia. Kuna haja ya kujenga Taifa bora, kuna haja ya kusema na kukaripia pale mambo mabaya kama haya yanapotokea, kuna haja ya kujenga Taifa jipya.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tunazungumzia mmomonyoko wa maadili. Mheshimiwa Waziri tukiwepo sisi viongozi, unatoka nyumbani asubihi unakwenda kazini, unarudi jioni kwa sababu ya foleni, hujui mtoto ameshinda na nani siku nzima, akiwa shuleni walimu wana msongamano wa wanafunzi wengi, mwalimu hawezi kuangalia tabia ya mtoto mmoja mmoja darasa lina watoto zaidi ya 50 au 60. Kwa hiyo, tunataka turudi nyuma sisi kama familia tuhakikishe tunafuatilia haki za watoto na makuzi yao ili tupate kuwa na Taifa bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, leo hii msichana wa kazi ndiyo anakuwa mlinzi wa mtoto nyumbani, Mama umerudi umechoka, baba amerudi na frustrations zake naye amechoka, huyu mtoto anajilea mwenyewe, anajifunza mwenyewe, wanaanglia pornographic pictures kwa sababu hakuna uangalizi nyumbani. Kisasa ambacho tumekuwa nacho, kizungu, tunaiga mambo ya magharibi, unamnunulia mtoto ma-toys ya kuangalia na wanajifunza mambo yasiyofaa.

Wakati mwingine tunaona sifa tunawanunulia watoto simu, unampa simu anakuwa na uhuru nayo, anakwenda ana- google anaanglia picha zisizofaa na wewe mzazi unafikiri ndiyo uzungu, unafikiri labda ndiyo maendeleo, mwisho wa siku tunaharibu watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunahitaji kujenga Taifa bora ambalo litafundisha watoto wetu umakini, kama inabidi, turudi zamani zile ambazo mtoto ni wa kijiji, mtoto ni wa mtaa, mtoto ni wa Taifa, anapokosea mtoto achapwe na jirani, aonywe na jirani, wala mzazi asiende kumgombeza mwalimu kwa nini umenichapia mwanangu ukome, huyu mtoto siyo wa kwako. Mtoto kwa sasa tunahitaji awe mtoto wa jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, rushwa ya ngono vyuoni. Tumeona mabinti wengi wakilalamikia suala la rushwa ya ngono vyuoni, wasichana wanaona bora basi kama ni hivyo hata kusoma wanashindwa wanajua mwalimu fulani ananihitaji basi nitatembea naye, naye atanipa GPA ya kutosha. Tunaomba Mheshimiwa Waziri kwa sababu wewe unahusika na Wizara hii, simamia nidhamu ya walimu wa vyuo.

Mheshimiwa Spika, kuna Mbunge hapa anayewakilisha vyuo vikuu amesema, mwalimu ni mdhamini mkuu wa mwanafunzi, lakini kama anataka ngono ili ampatie maksi anakuwa hatendei haki kazi yake na taaluma aliyosomea. Leo hii rushwa ya ngono imekuwa kilio kikubwa sana kwa wasichana na wanawake vyuoni, ninaomba wewe kama Waziri uweze kulisimamia hilo nasi tutakusaidia kupiga kelele katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, ukatili wa watoto wengi wameshausema. Mtoto mdogo ukatili unaanzia nyumbani. Leo hii nyumbani watoto wanaharibika tunazungumza suala la ushoga na mambo kama hayo, lakini asilimia kubwa inaanzia nyumbani. Leo hii tunaogopa kukaribisha mashemeji nyumbani, kaka zetu tunaogopa kuwakaribisha nyumbani kwa sababu utasema lala na uncle kule ndiyo uharibifu unakotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna namna kama Wizara inabidi tuzungumze, leo hii unajua unao majirani, majirani zako ni watu sahihi, lakini huyohuyo jirani yako unashangaa anatongoza binti yako na wewe uko palepale. Tunahitaji kupiga kelele kama Taifa. Ukatili wa kijinsia umekua mkubwa sana kwa sababu hata takwimu za 2022 ambazo zimezungumzwa na haki za binadamu, zaidi ya matukio 350 yamewakuta watoto wadogo. Leo tuna madawati lakini vijijini mpaka kufikia kwenye dawati la kijinsia ushahidi unakuwa umekwisha kupotea. Kuna haja ya kujitahidi sana kama Taifa kuweka ulinzi kwa watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine ninachoweza kushauri ni kwamba TASAF ipo kwa ajili ya kusaidia ustawi wa maisha ya watu. Mimi ninaomba TASAF ije katika Wizara yako, itoke kule iliko kwa sababu huku kwenye Wizara yako ndiyo sahihi ambako kuna uhitaji kusaidia watu katika ustawi wa maisha yao ya kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekwisha kusema hayo, lakini bado niendelee kusisitiza masuala ya makuzi ya watoto, kama Taifa lazima tuyapigie kelele. Leo hii mtoto analindwa na wewe mama, analindwa na wewe baba, ukisubiri Serikali ikusaidie, Serikali itakuja baadaye.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi nitoe rai kwa Watanzania wote, tunahitaji kuwalinda watoto kwenye maadili ya kidini, kila mtu ana dini yake amfundishe mtoto toka mdogo, kwa sababu tunaamini mtoto akiwa mdogo kichwa chake kinakua kinapokea vitu vipya. Kwa hiyo sisi tuseme nao, tunapokuwa tumechoka ni kweli tukirudi tukazungumze na watoto na tuwaonye watoto, tusiogope. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ninaamini katika sheria ya viboko japokuwa ipo, tuifwate hiyo sheria lakini itaweza kusaidia kubadilisha. Wengine tumefika hapa kwa sababu tulichapwa, tulionywa, tulikatazwa vitu vibaya, ndiyo maana leo tumefika mahali hapa. Tusianze kuiga mambo mengine kama Taifa tukaacha watoto wetu wanapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, mimi naunga mkono hoja kabisa katika Wizara hii kwa sababu mimi ni Mwanakamati na ninaona mambo mengi magumu ambayo Wizara hii inapitia na hasa tukizungumzia watoto ambao wako jela, tukizungumzia wazee ambao wamekosa makazi na Serikali hii inaamua kuwasimamia. Mimi naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Balozi Mulamula nafahamu sio mwanasiasa ni mtendaji nakumbuka bajeti ya mwaka jana alizungumzia atatekeleza suala la uraia pacha na kuileta kwenye bajeti hii, lakini hata hajazungumzia na wala hajaingiza kwenye bajeti yake. Kwa hiyo nataka tu kumkumbusha aendelee kuwa mtendaji asitufuate sisi wanasiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la viwanja, kiwanja cha Maputo kiwanja namba 157/1 wewe mwenyewe Naibu Spika ukiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Mambo ya Nje unafahamu ni kiwanja kipo zaidi ya miaka 40 enzi zile la Samora Machel na Julius Nyerere walipeana mpaka leo kiwanja kile hakijaendelezwa, hii imekuwa ni aibu kubwa sana kwa Taifa letu la Tanzania juu ya Balozi zinakuwa na viwanja vinakuwa vibovu popo wanaota mle kwenye majumba mabovu hii inajumuisha na nyumba kumi katika viwanja vitatu ambavyo vipo Zambia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mama Mulamula, Mheshimiwa kiongozi Waziri ukienda Zambia viwanja vyetu vipo prime area kabisa ambayo sisi kama Taifa tulikuwa tuna uwezo wa kuvijenga viwanja vile, mimi nina uhakika Msechu yule wa National Housing Cooperation alikuwa na uwezo mkamwambia akajenga pale na akijenga pale, Mheshimiwa Waziri ana uwezo wa kusaidia corridor ya Kusini yote tukaweza zile fedha ambazo zitapatikana pale zikaweza kusaidia Balozi zetu za Kusini mwa Afrika, lakini nashangaa majengo yameoza, majengo ni mabovu mpaka wanafikiria namna ya kutunyang’anya. Hii ni aibu sana kwa Taifa kama la Tanzania lenye uchumi ambao una uwezo wa kujenga balozi zile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na Balozi hizo wewe ni shahidi tunazo Balozi nyingi tumeshtakiwa majengo yanakuwa sio... Ufaransa kuna kipindi tulikuwa na jengo sio zuri sina uhakika kama mliendelea nalo na kulitengeneza.

Sasa Mheshimiwa nimesema wewe ni mtendaji sio mwanasiasa jitahidi kusimamie ile heshima yako uliyonayo ya kuisaidia Tanzania ikapata heshima ambayo tumedharaulika kwa muda mingi. Kiwanja kinakaa miaka 40 umri wa mtu anazaliwa anaoa anazeeka bado hatujaweza kukisaidia hicho kiwanja Mheshimiwa Spika naomba uingilie hilo, Naibu Spika naona na wewe kama kiongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda pale Abuja kuna kiwanja walitupa toka mwaka 1995 hadi leo wenzetu na kibaya zaidi kwa sababu mabalozi mnapopewa viwanja mnakuwa mpo wengi, kwa hiyo inaenda na lami inaenda vizuri, ikija kwenye Tanzania pana msitu unaenda tena sehemu nyingine Indonesia wananchi wamejenga Watanzani hatujajenga hii haiwezekani na wala haikubaliki…

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, muda wangu..

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji amekuwa anarudia maneno yake kwamba Mheshimiwa Waziri asiwe kama sisi wanasiasa. Sasa statement yake anatuchukulia wanasiasa wote hatuna credibility, kwani ni statement mbaya ya hovyo nataka nimwambie wana Siasa si kama wanavyojichukulia wenyewe, wengine ni wanasiasa tuna professionals zetu na tuna credibility, ahsante sana. (Makofi)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee, naona ndugu yangu alikuwa ana hamu ya kuchangia. Sipokei...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sophia, ngoja basi.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, sipokei...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sophia ngoja nikuite ndio nikwambie. Mheshimiwa Sophia, umeipokea taarifa?

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, sipokei naomba niendelee, naomba tuendele na suala la watumishi waliopo mabalozini najua kuna sheria ya utumishi unapompa mtu kazi akufanyie ni lazima uhakikishe stahiki zake zinakuwepo. Balozini kuna shida sana ya madai ya muda mrefu, kuna wafanyakazi wanadai unapowaongezea vyeo hawaendani sawa sawa na kipato wanachokipata, kuna madai ya nyuma ya safari na vitu kama hivyo tunaomba muwafanyie watu hawa stahiki zao ili waweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la diplomasia ya uchumi, tunashukuru Rais sasa hivi amerudi tena kwenye kuwasiliana na nchi mbalimbali tulikuwa tumepumzika kwa muda wa miaka kama sita, sasa ameamua kufungua upya. Ameenda kwenye Royal Tour na kweli tumeanza kuona mambo yakiendelea na wewe mwenyewe Waziri umesema kuna wafanyabiashara kama 100 kutoka Misri walikuja, na sisi hiyo tunaifurahia lakini pia Rais amefanya hiyo Royal Tour bado kuna shida kwenye mambo ya utalii ninajua kwamba mambo ya nje ya utalii vinaendana sambamba na hasa kwenye mambo ya hoteli. Kwa sababu utapata wageni sisi bado tupo chini sana kwenye industry ya kusaidia wageni tunaomba sasa wizara yako na Wizara ya Utalii kwa pamoja tusaidiane kusaidia wafanyabiashara wa kukaribisha hao watu ambao wanakuja kwa wingi tusipofanya vizuri hatutaweza kuingiza fedha na nguvu kubwa iliyofanyika tayari itakuwa imekwisha kupotea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Mabalozi mfanye kazi yenu ya kuhakikisha mnapochukua baadhi ya wafanyabiashara hapa na kuwapeleka nje wakaone wenzao wanafanya biashara vipi hasa za hoteli kwa sababu tunahaja na tunakaribia kupokea wageni wengi sana na bado industry yetu ya hoteli haijawa nzuri, watu wameendelea kuwa wavivu, watu hawafanyikazi kwa kujituma. Tayari wageni wanakuja ukipata wageni 100 na wewe unaanda chai saa nne badala ya saa mbili iwe tayari, tayari unakosa wateja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kwenye suala la hiyo hiyo diplomasia ya uchumi; umesema kuna mtandao wa jb.com kule China ambao unaangaliwa na watu takribani milioni mia saba umesema, hawa ni watu wengi sana, lakini bado sisi pamoja na corona, lakini bado Tanzania kule Guangzhou ambao ndiyo mji wa kibiashara tulikuwa hatuna Balozi ndogo pale ni mpaka waende kwenye Balozi kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mji ukishakuwa wakibiashara lazima ujiongeze wewe kama nchi, tunafahamu nji ya jirani zetu sitaki kuwataja, wao hadi kwenye mabasi ya wachina kuna matangazo yao sisi tunashindwa nini! Mimi nimesema hapa kuna mmoja amesema nisikuambie wewe mwanasiasa bado ninakwambia mtu ambaye ni mtendaji haongei lugha mbili, ninaomba usimamie hilo uhakikishe kwamba tunaweka nguvu mpya ya kibiashara Guangzhou na tunapeleka matangazao mengi Guangzhou, tuhakikishe tunafanya biashara ya Guangzhou ili tuweze kukuza diplomasia ya uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya ninaendelea kuomba, ninaomba mama yangu chapa kazi, usimamie yale unayoyaamini kama nilivyosema wanawake wakiamini jambo lao wanalifanyia kazi, ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia kwenye mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninashukuru hii Idara ya Mipango imerudi tena kwa sababu ilikuwepo baadae ikatoka Mheshimiwa Rais ameirudisha tena na ametupatia Waziri kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yoyote au hata ngazi ya familia pasipokuwa na mipango thabiti siyo rahisi kabisa kufikia malengo makubwa ambayo familia hiyo au nchi hiyo imejipangia. Tanzania tulikuwa na usemi ambao naamini bado tunaendelea nao kwamba kilimo ni uti wa mgongo. Mimi naamini kwamba bado tunaendelea nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa asilimia zaidi ya 80 au ikishuka sana asilimia 75 bado tunaendelea na suala la kilimo na wananchi wengi ni wakulima. Bado sijaona jitihada kubwa sana ya kuhakikisha tunakuwa na kilimo chenye tija. Pamoja na kuongeza bajeti kwenye Wizara hii bado kilimo chetu hakiendani na ufasaha kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilizungumzia kuwa na kilimo cha kimkakati na safari hii tulizungumzia zao la alizeti, wananchi wakahamasika, wakaanza kulima alizeti, mpaka sasa alizeti imejaa kwenye maghala bado imeshuka bei wananchi wamebaki wanashangaa, kwa sababu tunafahamu kwamba mkulima anapolima lazima anakuwa na malengo yake. Leo hii kama tunakuwa na maghala alizeti imejaa na bado tunaingiza alizeti nyingine toka nje inabidi tujue mipango kama Taifa tunataka nini. Tumewaambia wakulima walime alizeti wakati huo huo tunaingiza alizetu toka nje lazima soko litayumba na anayeumia zaidi ni yule mkulima ambaye yeye kodi inambana na yule anayeleta toka nje ana unafuu wa uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la alizeti nimelisema lakini tunalo zao la parachichi. Tunaita parachichi ni dhahabu ya kijani, leo hii mkulima wa parachichi anahangaika na zao hili, analima lakini mwisho wa siku bado hatujapata masoko ya parachichi. Jirani zetu wa karibu wanakuja wananunua kwa bei ya kutupa kwa mkulima kule chini lakini wanavusha nje ya nchi, wakienda kwenye nchi zao wanaotuzunguka wana-brand kama yale maparachichi yametoka katika nchi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Taifa lazima tumtetee mkulima tuhakikishe zao hili anapolima liwe lina tija na limletee faida yeye na familia yake lakini mwisho wa siku Taifa lipate faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na kilimo kisichokuwa na masoko, tunakuwa hatujamtendea haki Mtanzania, ni lazima tutafute masoko. Leo hii Tanzania imekuwa nchi ambayo wanalima alizeti, wanalima ufuta, wanalima mazao kama hayo lakini mwisho wa siku wanakuja kununua madalali na kwenda kuuza nje wakati sisi bado tunayo nafasi. Nimesema kilimo cha tija, leo hii ukienda kwa nchi zetu jirani heka moja ina uwezo wa kutoa magunia 40, sisi tukitoa magunia mengi ni magunia 10! Lazima tubadilike katika kuhakikisha tunatetetea mazao ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tumepata wito wa kulima mbaazi, tunafahamu sote miaka mitatu iliyopita tulitangaza mbaazi kwamba ina soko Nchi ya India na wananchi wakalima, mwisho wa siku tuliambiwa tule kama mboga, haiwezekani! Ni lazima tuwe na mikakati ambayo inamsaidia mkulima wa kawaida akiambiwa anaiamini Serikali yake kwamba ninachokifanya kinaenda kutimia kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ya kuyaangalia, kwa mfano migogoro ya ardhi pia, hatuwezi kuwa na nchi yenye mipango wakati huo hatuwezi kuitumia vema ardhi yetu. Leo hii kila siku tunazungumzia migogoro. Hakuna namna bora ya kuwasaidia wananchi hasa kwenye mambo ya ardhi, mkulima ajue ana ardhi yake kiasi gani, lakini mfugaji nae aelekezwe ni sehemu gani atasimamia, tutaishia kukaa kwenye migogoro na kuweka miongozo na kulalamika kama Wabunge wakati Wizara husika ipo tunaomba muweke msisitizo katika utunzaji wa ardhi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TMA wametuambia habari ya mvua, kwamba kuanzia Oktoba mpaka Disemba tutakuwa na mvua. Mimi ninaiomba Serikali ihakikishe inanunua mazao kwa wingi. Tunafahamu mna uwezo wa kununua tani milioni tatu, lakini maghala mliyonayo yanaweka tu tani laki tano na inayobaki tani milioni mbili na laki tano ni kwa watu binafsi. Ni hatari sana kutegemea watu binafsi katika uhifadhi wa chakula wakati Serikali ipo. Tunaomba mnunue chakula kama haya majanga yataendelea na sisi tunamwomba Mungu yasitokee yashindwe, lakini mwisho wa siku lazima tujiwekee akiba na akili ya kuhifadhi chakula chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini kama mvua itaendelea kusumbua mwisho wa siku tutakosa chakula hapo mbele kwa maana mazao yatakuwa hayawezi kuwa sawa sawa, lakini kwa sehemu zile ambazo mvua haijaharibu tunaomba mbolea iende kwa wakati, wananchi waweze kulima mapema labda itaenda kutuokoa kwa hiyo nafasi iliyobaki. Mheshimiwa Waziri husika wa Mipango hakikisha unamlinda mkulima na kumuwekea mipango thabiti ambayo itamsaidia katika ukulima wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunategemea kilimo hatujajitoa kwamba sisi ni mabepari, bado sisi ni wakulima, sisi ni wafugaji na asilimia zaidi ya 70 ni watu ambao wanaendelea kwenye kilimo. Ninaomba utuwekee mkazo uthabiti katika kulinda haya. Hili suala la mvua ambalo linaendelea na ambalo tumeambiwa na TMA tusilidharau, tuhakikishe tunaongeza idadi ya kununua chakula kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninaomba majibu Mheshimiwa Waziri atakapokuja tunaongeza kiasi gani cha tani cha ununuzi na kujenga miundombinu ya kuifadhi maghala ya chakula. Ahsanteni. (Makofi)