Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Abdallah Hamis Ulega (1 total)

MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, hapo nyuma kidogo Serikali ilitoa agizo kwa nia njema kabisa ya kutaka kutunza na kuboresha mazingira yetu, agizo lenyewe lilitutaka wananchi maeneo mbalimbali katika nchi kuhakikisha kwamba mwishoni mwa wiki tunafanya usafi wa mazingira.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, jambo hili ni jema sana na sisi wananchi tulilipokea vizuri sana katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Jambo hili limesababisha kero na usumbufu mkubwa kwa wananchi, hasa kwa kufungwa huduma muhimu wakati wanapokuwa wanazihitaji, huduma kama vile vituo vya afya, zahanati hata mahospitalini asubuhi ya siku ya Jumamosi wananchi wamekuwa hawapati huduma ipasavyo, migahawa pia katika maeneo ya miji imekuwa ikifungwa.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, je, Serikali ipo tayari sasa kutoa ama kuboresha agizo hili ili wananchi wale waendelee kupata huduma ipasavyo wakati huu wa asubuhi wa mwisho wa wiki?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka msisitizo wa nchi yetu kuwa safi kwenye maeneo tulimo, kwenye makazi, maeneo ya jumuiya, maeneo ya utoaji huduma ili kuifanya nchi kuwa safi kama ambavyo sasa tunaona maeneo kadhaa yana usafi unaoridhisha lakini bado tunatakiwa tuongeze nguvu. Utaratibu ambao tumeutoa ni kwamba tumekubaliana nchi nzima kila Jumamosi moja ndani ya mwezi mmoja kadri Mikoa ilivyojipangia au Wilaya ilivyojipangia ni kwamba Watanzania wote lazima tujihisishe kwenye usafi wa maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika makazi yetu lakini na maeneo ya jumuiya kama vile vituo vya mabasi, hospitali na maeneo mengine. Utaratibu unaendelea, Mheshimiwa Mbunge ameomba kujua utaratibu unaotumika na baadhi ya maeneo wa kufunga maeneo muhimu, nasi tumesisitiza kwamba viongozi wa maeneo hayo ambao wanatambua kwamba eneo hili ni la utoaji huduma za jamii ambao ni muhimu, waweke utaratibu mzuri wa namna ya utoaji huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu suala la usafi ni kuanzia saa 12.00 na tumesema angalau mpaka saa 4.00 asubuhi, kwa hiyo ni kwa saa manne tu. Kama eneo hilo linaweza kuvumilika kusitisha kwa muda fulani ili kuruhusu kufanya usafi ni vizuri, lakini kama eneo hilo lina mahitaji makubwa ya utoaji wa huduma basi Mkuu wa Wilaya, Mwenyekiti wa Kijiji na viongozi wa maeneo hayo waweke utaratibu mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, viongozi wanaosimamia zoezi hili waangalie umuhimu wa utoaji huduma wa maeneo ya jumuiya kama ni lazima yafungwe kwa saa manne hayo au vinginevyo ili kuruhusu kufanya usafi. Kwa mfano maeneo ya hospitali hatuwezi kuyafunga hili eneo lazima liwe wazi wakati wote kwa sababu tunazo dharura zinaweza kutokea wakati wowote. Hivyo muhimu zaidi ni kuweka utaratibu wa usafi wake kwanza kabla ya siku ya Jumamosi ili Jumamosi huduma ziweze kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya migahawa yenyewe wakati wote yanatakiwa yawe safi hata bila kuwa na Jumamosi, ni muhimu zaidi wale waendesha migahawa wahakikishe maeneo hayo yanafanyiwa usafi vizuri na siku ile ya Jumamosi kama kiongozi wa eneo hilo anaona kuna umuhimu wa eneo hilo kutofunga ili shughuli ziendelee basi tujiridhishe kwamba eneo hilo liko safi, kwa vile usafi ule unajumuisha wananchi wote kwa pamoja kutoka kwenye eneo hilo, watumishi wa eneo hilo waingie kwenye usafi kwa pamoja ili waweze kushiriki kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu zaidi ni kiongozi wa eneo hilo kuona umuhimu wa eneo hilo na mahitaji yake, aweke utaratibu mzuri kwa ajili ya kufanya kazi bila kuzuia huduma nyingine kuendelea. Ahsante.