Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Abdallah Hamis Ulega (25 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuzungumza katika Bunge lako hili Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nichukue fursa hii adhimu kabisa kuwashukuru sana wapiga kura wangu wa Jimbo la Mkuranga katika Mkoa wa Pwani, naomba niwahakikishie ya kwamba kazi yao walionituma ya kuwawakilisha nitaifanya kwa weledi, uaminifu, juhudi na maarifa yangu yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizi, nami kwa kuwa sikupata fursa ya kujadili hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa hapa katika Bunge lako hili Tukufu, naomba nichukue fursa hii pia kusema kwamba hotuba ya Mheshimiwa Rais ilimaliza kazi yote, nami binafsi baada ya pale nilifanya ziara katika Jimbo langu la Mkuranga kwa ajili ya kutoa shukrani na Wanamkuranga wana imani kubwa sana na Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli. Wanasema Mheshimiwa Rais aendelee na kazi yake na imani yetu ya kuiona Tanzania ikielekea katika uchumi wa kati ni kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niendelee katika hoja hii inayohusu Mpango wa Maendeleo ambayo imetolewa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha hapa Bungeni. Kwanza kabisa ningeenda kugusa katika eneo la viwanda. Mkakati wa Serikali yetu ni mzuri, na mimi binafsi nauunga mkono kwa asilimia 100. Hata hivyo, yapo mambo ambayo ningefikiri kwamba hatuna budi kujielekeza kuona ni namna gani tunajipanga nayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la viwanda, pale Mkuranga, neema ya viwanda imeshaanza kuonekana. Tunavyo viwanda vingi sana sasa ambavyo vinajengwa kila kukicha. Sababu yake kubwa ni pamoja na kwamba Dar es Salaam imeshajaa na sasa inapumulia katika Wilaya ya Mkuranga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii kwetu imekuwa ni faraja kubwa sana na tungeomba jambo hili liendelee na hata Serikali iendelee kutusaidia kuhamasisha kuhakikisha kwamba wawekezaji wa viwanda mbalimbali wanaendelea kumiminika pale katika Jimbo letu hili la Mkuranga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango mkakati wa maendeleo uliopita, wakati tunaujadili utekelezaji wake, Mheshimiwa Waziri wa Fedha alisema neno, kwamba katika mambo yaliyotufanya tushindwe katika uwekezaji wa viwanda hapo nyuma ni pamoja na fidia za ardhi. Fidia ya ardhi ipo kwa mujibu wa Sheria namba 4 ya mwaka 1999, lakini ninalo jambo ambalo nilikuwa nikilifikiri sana na nilikuwa nafikiri kwamba wataalam walichukue wakalijadili, waone ni namna gani tunaweza tukaboresha kitu cha namna hii. Hizi fidia za ardhi zimekuwa zikifanywa kila mara, lakini kama fidia ya ardhi inayohusu biashara, hasa ya viwanda na sisi tunataka uchumi wa viwanda kuelekea uchumi wa kati umilikiwe na Watanzania wenyewe, nafikiri tuanze kubadilisha mtazamo wetu. (Makofi)
Watanzania wamekuwa wakipewa fidia, si jambo baya, ni haki ya kisheria, lakini wakishapewa ile fidia, wanaelekea wapi. Tumeona watu wakipewa fidia Dar es Salaam, kule Kibada, Kigamboni watu wanalipwa fidia vizuri sana tu wanakwenda na sisi pale Mkuranga tutalipwa fidia, lakini baada ya hapo tunasogezwa, tunaondoka. Sasa tutasogea mpaka tutafika Rufiji, tukitoka Rufiji tutakwenda mahali pegine, ardhi ile tumepoteza na uchumi ule hatutaendelea kuumiliki. (Makofi)
Wazo langu nililokuwa nafikiri ni kwamba, ni lazima itafutwe mbinu nzuri zaidi ya kuwafanya Watanzania hawa wawe ni sehemu ya umiliki wa vile viwanda, wao mchango wao uwe ni ile ardhi yao. Tuliweke jambo hili vizuri badala ya kuja kuwapa fidia ya 1,500,000. Anaondoka Mtanzania yule wa pale Mkuranga, ameacha kiwanda kimetengenezwa pale, ile haitamsaidia. Kama ungetengenezwa mpango madhubuti na mzuri, maana yake ni kwamba eneo lake linakuwa ni mchango katika kiwanda kile atakula yeye, watoto wake, wajukuu wake na mpaka vitukuu vyake! Nadhani hii itakuwa ni namna bora zaidi ya kuwafanya Watanzania wamiliki uchumi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala hilo la viwanda, nimewahi kuzungumza kwamba pale sisi tunavyo viwanda vingi lakini viwanda hivi lipo tatizo la ajira, ajira zile zinazotolewa tunasema kwamba sio decent. Hazina staha! Vijana wetu wako wengi kweli wanapata vibarua mule ndani, ajira zile ndani ya saa kumi na mbili hawapumziki hata kidogo. Baada ya hapo analipwa 4,500, lakini ni ajira hatarishi kwelikweli. Naomba jambo hili wakati tunaendelea kuomba hivi viwanda tuliangalie vizuri ili tujiandae nalo lisije likatuletea matatizo hapo mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mkakati wa maji ambao umesemwa na Waheshimiwa Wabunge wengi kwamba maji ni uhai na Mbunge mwenzangu wa Rufiji amesema vizuri sana hapa mchana huu wa leo juu ya suala la maji. Kutoka Rufiji, Mto Rufiji mpaka Mkuranga, hazizidi kilometa 100. Maji kule yamekuwa ni mengi mno yanaleta hata mafuriko! Tusaidieni tuondokane na tatizo la maji na liwe ni historia. Yatoeni maji kutoka Mto Rufiji, yafike Mkuranga, yapite Kibiti, Ikwiriri, Bungu na maeneo mengine ya Wilaya zetu hizi. Mkifanya hivi mtakuwa mmetusaidia sana. (Makofi)
Vilevile upo mkakati wa maji mkubwa pale katika Kijiji cha Kisemvule, ningeomba maji ya pale Mpera yasiondoke kwenda Dar es Salaam mpaka kwanza na sisi watu wa Mkuranga tuwe na faida nayo maji yale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunaendelea kuangalia namna ya kuboresha uchumi wetu, naomba nizungumzie miundombinu. Wilaya ya Mkuranga kama tulivyosema, Jimbo letu hili lipo kabisa kimkakati kwamba ni sehemu ya kupumulia katika Jiji la Dar es Salaam. Ombi langu hapa ni kuhakikisha kwamba pesa katika Mfuko wa Barabara ziongezeke. Ziongezeke ili tuweze kutengeneza miundombinu yetu. Sisi pale tuna uchumi mzuri, lakini uchumi ule umekwama kwa sababu miundombinu ya barabara katika Jimbo hilo ni mibaya sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwenzangu wa Rufiji alisema kwamba Rufiji katika umri wake wote toka iwe Wilaya hata nusu kilometa ya lami hakuna, sisi hata robo kilometa ya lami haipo katika Wilaya yetu ya Mkuranga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono hoja hii ya Mpango wa Maendeleo wa mwaka mmoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nichukue fursa hii kukushukuru sana kwa nafasi hii niliyopata ya kuchangia Mpango huu wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambao unaenda kuleta matumaini makubwa ya Tanzania yetu mpya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba pia nichukue fursa hii kwa haraka haraka kumshukuru na kumpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kasi kubwa na nzuri anayokwenda nayo na hasa hii ya kutumbua majipu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sisi tunasema kwamba Mheshimiwa Rais aendelee kusonga mbele na sisi tupo pamoja naye maana katika nchi hii kama kuna watu ambao wametuangusha kwa kiasi kikubwa na kwa muda mrefu ni watumishi. Wametuangusha kwa muda mrefu na watu walikuwa wanahisi kwamba labda wao ni watu wasioguswa. Napenda kusema Mheshimiwa Rais anaendelea kuwapa hata Waheshimiwa Mawaziri wetu ujasiri wa kufanya kazi na sisi Wabunge na Watanzania kwa ujumla wake tunawaunga mkono. Lazima twende mbele zaidi ikiwezekana tuiangalie Sheria yetu ya Utumishi maana huko watu ndipo walipokuwa wanajifichia wakihisi kwamba hawana namna ya kuweza kuguswa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya, naomba sasa nielekee katika kuzungumzia Mpango wetu wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambao unakwenda sambamba na uchumi wa viwanda ili kuelekea katika uchumi wa kati.
Mheshimiwa Spika, jana nimesikitika sana katika Hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani rafiki yangu mwasilishaji kaka yangu Mheshimiwa David Silinde alikuwa anakatisha tamaa suala la viwanda na akafika mahali akazungumzia mpango ule wa Serikali wa kuanzisha industrial business hub pale Kurasini kwa kusema kwamba kwa kufanya vile ni kama tunakaribisha Wachina sisi tunajigeuza kwenda kuwa wachuuzi, nadhani hajaelewa vizuri jambo hili.
Mheshimiwa Spika, namwambia Waziri wa Fedha aharakishe sana ile Kurasini business hub ipatikane kwa haraka. Wachina kule kwao wanafunga vile viwanda wanakuja kufungua hapa Tanzania. Namkaribisha aanze kuona namna Wachina wanavyokimbilia hapa Tanzania kufungua viwanda pale Mkuranga, tuna viwanda vingi na vinajengwa kila siku ya Mwenyezi Mungu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hivi sasa kiwanda kikubwa cha tiles kinajengwa pale Mkuranga katika Kijiji cha Mkiu. Kile kiwanda cha marumaru kitalisha East Africa nzima. Tutakapopata business hub pale Kurasini maana yake ni kwamba watu watakuwa wanajua one business stop center ipo pale Kurasini na watakwenda kupata bidhaa zinazozalishwa pale. Sisi leo pale tuna viwanda vya cement wenzangu wa Mikoa ya Kanda ya Ziwa wanaomba viwanda vya cement. Tuna kiwanda cha cement cha RHINO, tuna kiwanda cha cement cha Diamond pale, tunatengeneza mpaka yeboyebo pale Mkuranga.
Mheshimiwa Spika, kwa bahati njema sana bomba la gesi lipo pale na namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Viwanda Mheshimiwa Mwijage kwa namna ambavyo ananipa support kubwa ya kuwaleta wawekezaji waje kuwekeza katika lile bomba la gesi ambalo lina toleo lake katika vijiji vyangu vya pale Mkuranga. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba niendelee kuunga mkono…
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nasema Serikali iendelee na mpango huu wa viwanda na sisi tumejipanga vizuri sana. Katika eneo moja ambalo tumejipanga vizuri pale Mkuranga ni hilo la viwanda, tuna hekari zaidi ya elfu kumi ambazo zipo tayari kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nipongeze sana Mpango wa Serikali wa Miaka Mitano ule wa kuboresha miundombinu yetu. Katika hili naomba nimwambie rafiki yangu Mheshimiwa Silinde na Kambi Rasmi ya Upinzani namna alivyopotoka tena amemtaja mpaka kipenzi chetu Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika ukurasa wa tisa eneo la barabara, eti Kambi Rasmi ya Upinzani inapenda kuwakumbusha Watanzania kwamba aliyekuwa Waziri wa Ujenzi wakati wa utekelezaji wa mpango uliopita ndiye Rais wa sasa, kwa hiyo hakuna matumaini. Nataka nimwambie matumaini ni makubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwanza katika takwimu zake nataka nimwambie amekosea jambo moja kubwa. Waziri wa Fedha alipokuwa anasoma Mpango ule ametuelekeza kwamba mpango wa Serikali ulikuwa ni kujenga kilometa za lami 5,775 lakini mpaka tunafika Desemba 2014 zilikuwa zimeshajengwa zaidi ya kilometa 2,775. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hapa Waziri wa Fedha hakuweka mwaka wa 2015, kuanzia Desemba, 2014 mpaka 2015 na kufika hapa leo, Wizara ya Ujenzi katika muda huo ambao haukutajwa imejenga zaidi ya kilometa 500 za barabara za lami. Naomba nizitaje, Ndundu - Somanga kilometa 60, Tunduma - Sumbawanga kilometa zaidi ya 200, Lwanjilo - Chunya kilometa zaidi ya 36 na Iringa - Dodoma zaidi ya kilometa 259. Kwa namna ya kipekee kabisa naipongeza Serikali yangu namna tulivyojenga barabara za lami za kupunguza msongamano katika Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba niitaje barabara ya Ubungo Bus Terminal…
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mpaka Mabibo na Kigogo zaidi ya Kilometa 6.4, barabara ya kutoka Uwanja wa Ndege pale Jeti kwenda Vituka mpaka Devis Corner kilometa zaidi ya 10, barabara ya kutoka Ubungo Maziwa - External zaidi ya kilometa 2.25, barabara ya kutoka Kibamba - Mloganzila zaidi ya kilometa 4. Halafu watu hawa namna wasivyokuwa na shukrani tazama ukipita leo katika Jimbo la Ubungo unatoka Goba mpaka unakwenda kutokea Chuo Kikuu ni lami tupu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, namwomba Waziri wa Fedha katika Mpango huu aoanishe na Waziri wetu wa Ujenzi sasa twende katika kuijenga barabara ya kutoka Mkuranga - Kisiju ambapo eneo hilo linakwenda kuwa la viwanda. Hii ni katika kukamilisha ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipokuja kuwaomba kura Watanzania wale wa Mkuranga aliwaambia barabara ile itajengwa. Nina hakika kwa mwendo ambao tunakwenda nao barabara ile itajengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba sasa nielekee katika maji…
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Spika, nasikitika sana kusema kwamba muda wote huo ….
SPIKA: Mheshimiwa Ulega kuna taarifa ngoja uipokee.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Haya ahsante.
SPIKA: Mheshimiwa Silinde kifupi sana....
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Spika, sijaipokea kwa sababu rafiki yangu Mheshimiwa Silinde nimemkumbusha kwamba ujenzi wa barabara uliendelea katika mwaka wa 2015, asisahau na madaraja ambalo na yeye atakwenda kupigia picha pale Kigamboni. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, nasikitika kusema kwamba wenzetu hawa hata masuala ya maji hawakuyazungumzia. Tazama Serikali yetu ina mpango mzuri sana wa maji.
Mheshimiwa Spika, katika hili la maji, napenda niipongeze sana Serikali. Napenda niseme kwamba nina hakika katika miaka mitano hii ile ajenda yetu ya kumshusha mama ndoo kichwani itafanikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mpango wa Maendeleo unaelekeza kwamba katika miaka mitano iliyopita takribani asilimia zaidi ya 60 ya Watanzania walipata maji safi na salama. Katika Jiji la Dar es Salaam, watu wanabeza tazama Jiji la Dar es Salaam lilivyopata bahati kubwa sana tena kwa pesa zetu wenyewe za ndani. Maji ya kutoka Ruvu Chini yamepita Bagamoyo yamekwenda mpaka Chuo Kikuu kule cha Dar es Salaam, bomba lile limelazwa kwa pesa ya Serikali yetu. Kwa kweli napenda sana niipongeze Serikali. Pia kuna mpango wa maji wa Dar es Salaam wa Ruvu Juu ambao sasa hivi unaendelea vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pale Mkuranga upo mradi mkubwa wa maji ambao utahudumia Dar es Salaam kwa maana ya maeneo ya Kigamboni, Mbagala na Kisarawe, mradi ule wa Kimbiji na Mpera. Naiomba Serikali sasa ihakikishe kwamba mradi ule unawanufaisha na watu wa Mkuranga katika vijiji vya Mkuranga, Dundani, Mwanambaya, Mwandege, Kipala Mpakani vyote viweze kupata maji yale. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niishauri Serikali katika Mpango huu wa Miaka Mitano ihakikishe kwamba inatoa maji kutoka katika Mto Rufiji kwani zaidi ya asilimia 50 ya maji ya Mto Rufiji hayana matumizi yoyote. Kilometa hata 200 hazifiki kutoka Mto Rufiji kuja Dar es Salaam. Tuyatoe maji yale tuyalete Dar es Salaam, maji haya ya visima hayana hakika hata Naibu Waziri wa Maji jana alieleza hapa, Engineer Kamwelwe yeye mwenyewe amesema kwamba maji haya ya visima hayana hakika.
Mheshimiwa Spika, tutakapotoa maji kutoka Mto Rufiji yatanufaisha Wilaya za Rufiji, Kibiti, Mkuranga na yatanufaisha Dar es Salaam yote ya Kusini bila kuisahau Kisarawe. Naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha aweke mpango huu madhubuti wa kuhakikisha tunatatua kabisa kero ya maji katika Wilaya zetu na nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mwisho, naomba nizungumzie suala la kilimo. Katika Mpango wa Maendeleo imeelezwa kwamba kutoka 2010 kurudi nyuma ilikuwa ni karibu asilimia mbili na point lakini kutoka 2010 kuja 2015 zilizidi kidogo asilimia ikaja mpaka asilimia 3.4 bado ukuaji huu ni mdogo. Pamoja na ukuaji huu kuwa mdogo bado nchi yetu imekuwa na chakula cha kutosha na mpaka tukawa na chakula cha ziada.
Mheshimiwa Spika, hivi sasa tuna tatizo kubwa la mabadiliko ya hali ya hewa, naiomba sana Serikali katika mpango wake wa bajeti hii tunayokwenda nao sasa ihakikishe kwamba mambo makubwa mawili, matatu yafanyike.
Mheshimiwa Spika, la kwanza, ni kuipa nguvu zaidi Wizara yetu ya Kilimo ili tuweze kujielekeza zaidi katika kilimo cha umwagiliaji. Hata pale kwangu Mkuranga ipo miradi ya umwagiliaji ya Changanyikeni, Yavayava na Kisere. Miradi ile yote haiendi vyema ni kutokana na ukosefu wa fedha. Ninayo matumaini makubwa kwamba katika mwaka huu tunaokwenda nao tutapata pesa ya kutosha na hatimaye miradi ile inaenda kutekelezwa na kukamilika na kuwanufaisha wananchi wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la pili, ili kuhakikisha kilimo chetu kinaenda vizuri ni pembejeo. Ni lazima tuipe pesa ya kutosha pembejeo ili kilimo chetu kiwe na tija. Kwangu naomba sana pembejeo ya sulfur. Pembejeo hii ya sulfur nashauri iuzwe kama inavyouzwa cocacola dukani. Sisi wakulima wa korosho tukikuta sulfur inauzwa kwa wingi madukani tutaridhika sana. Nataka nikuhakikishie wakulima wote wa korosho baada ya hapo tutakipa chama chetu Chama cha Mapinduzi kura zote za ndiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tuna matumaini mkubwa sana, tazama mfumo wetu wa stakabadhi ghalani, Waziri Mkuu juzi amekwenda kule Mtwara na Lindi ameboresha mfumo huu. Tunayo matumaini kwa kasi tunayokwenda nayo kero zote zinazotusumbua katika mfumo wa stakabadhi ghalani zitatatuliwa. Mwaka huu korosho imeuzwa zaidi ya Sh.2,500 kwa kilo katika Wilaya yangu ya Mkuranga. Watu wamepata pesa nyingi na mambo yanakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niunge mkono hoja ya Mpango huu wa Maendeleo. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Awali ya yote napenda kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunifikisha hapa nilipo leo nikiwa na afya njema. Nianze mchango wangu kwa kutamka kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kujibu hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge, naomba kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. Napenda kutumia nafasi hii kumuahidi Mheshimiwa Rais kwamba nitafanya kazi yangu kwa uadilifu na uaminifu mkubwa sana ili kuhakikisha kwamba Tanzania sekta hizi za mifugo na uvuvi zinachangia kikamilifu katika kuinua pato la mfugaji na mvuvi na kuipeleka Tanzania kwenye uchumi wa kipato cha kati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napenda nichukue fursa hii nimshukuru tena Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa kwa uongozi wao mahiri na makini kabisa ambao unaipeleka nchi yetu katika uelekeo wake ule ule wa amani, utulivu na maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kumshukuru Waziri wangu Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina, Mbunge wa Kisesa kwa kunishirikisha kwa karibu sana katika majukumu ya kuongoza Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Spika, pia nikushukuru sana wewe mwenyewe, Naibu Spika, Wenyeviti wote wa Bunge, Wabunge wa Kamati ya Kilimo, Mifugo na Waheshimiwa Wabunge wote kwa ushirikiano wao kwa ujumla wanaonipa katika utendaji wangu wa kazi za ndani na nje ya Bunge letu tukufu. Nawaahidi ushirikiano na nasema ahsanteni sana kwa ushirikiano mnaonipa kila mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia vilevile nichukue fursa hii niwashukuru watendaji wetu katika Wizara, Katibu Mkuu Dkt. Mary Mashingo anayeshughulika na mifugo, vilevile Katibu Mkuu Dkt. Yohana Budeba anayeshughulika na uvuvi na Wakuu wa Idara zote na taasisi zote zilizoko katika wizara yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nichukue fursa hii kuwashukuru sana wapiga kura wangu katika Jimbo la Mkuranga na nataka niwahakikishie kwamba mimi kijana wao niko makini na timamu kabisa kuendelea kuitumikia kazi hii ya Ubunge wa Jimbo la Mkuranga bila ya kuchoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee, naomba uniruhusu pia nimshukuru mke wangu na familia yangu kwa namna ambavyo wamekuwa wakinipa ushirikiano wa hali na mali wakati wote wa kutumikia kazi hizi za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya, naomba sasa uniruhusu niweze kujibu hoja ambazo zimeletwa na Waheshimiwa Wabunge wakati wakichangia mjadala wa bajeti yetu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Kwanza, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote, sisi katika Wizara tumeyachukua mawazo, maoni na maelekezo yao mbalimbali waliyotupatia. Nataka niwahakikishie kwamba vitu vyote hivi walivyotushauri tutavifanyia kazi ili kuweza kupata uendelevu wa sekta zetu hizi za mifugo na uvuvi kwa manufaa mapana sana ya nchi yetu ya Tanzania. Mimi nitazungumza kwa uchache lakini baadae Mheshimiwa Waziri wangu atakuja kueleza kwa upana zaidi ili kuweza kujibu hoja zote bila mashaka yoyote yale.

Mheshimiwa Spika, la kwanza ambalo limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi ni namna ambavyo sisi kama Serikali tulivyojipanga kuhusiana na sekta hii inayochipukia ya ufugaji wa samaki. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge sisi tunaelewa namna ambavyo Wabunge wengi wamekuwa wakivutiwa na suala hili la ufugaji wa samaki kwa maana ya aquaculture. Mpango mkakati wetu ni kuhakikisha kwamba Watanzania walio wengi wanaingia katika ufugaji wa samaki kwa sababu ufugaji wa samaki umekuwa ni wenye kuleta matumaini.

Mheshimiwa Spika, namna gani Wizara tumejipanga? Nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge, sheria na kanuni zetu wakati fulani unaweza ukaziona kwamba, mathalani samaki ambao wanafugwa katika mabwawa yetu hawaruhusiwi kuchakatwa na hata kuuzwa nje. Hivi ni vitu ambavyo vimesababisha wakati mwingine sekta zetu zisisonge mbele kwa sababu zinakuwa si sekta shindani, watu hawavutiki kwenda kuwekeza pesa zao katika aquaculture.

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie baada ya mazungumzo ya muda mrefu chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Waziri Luhaga Joelson Mpina, tumekubaliana kufanya mapinduzi katika eneo hili la aquaculture. Moja, hatuoni sababu ya kwa nini samaki wanaozalishwa katika mabwawa yetu wasiuzwe kibiashara. Kwa hiyo, nataka niwaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba eneo hili tunakwenda kulifanyia marekebisho. Tuchakate samaki wetu wanaotoka katika mabwawa (ponds) lakini turuhusu pia vilevile hata wauzwe ili tuweze kuvutia uwekezaji zaidi kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, kama hilo halitoshi tumeona juu ya kodi na tozo mbalimbali ambazo zinafanya sekta hii isiweze kuvutia hasa katika eneo la uingizaji wa vifaa mbalimbali. Tumekuwa tukiendelea na mashauriano na wenzetu wa Wizara ya Fedha, tunaamini kwamba watalifanyia consideration ambayo itakwenda kuwasaidia Watanzania wavutike katika kuwekeza kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumejiwekeza zaidi katika kwenda kuviimarisha vituo vyetu, tunavyo vituo nchi nzima vinavyofanya kazi hii ya aquaculture. Vituo vyote hivi tumejielekeza katika kwenda kuviimarisha ili kuzalisha vifaranga vya kutosha, tuvigawe kwa wananchi lakini vilevile kuhakikisha tunapata chakula bora kwa ajili ya ufugaji wa samaki. Maana tatizo kubwa lililopo katika eneo hili ni upatikanaji wa chakula kizuri na upatikanaji wa vifaranga. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba vyote hivi tunaenda kuvitatua.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo limezungumzwa na Wabunge wengi ni eneo la nyavu, je, hizi nyavu mbona zimekuwa na mjadala mkubwa sana, ni nini tatizo? Pia vilevile imezungumzwa ya kwamba sisi tumetoa monopoly ya kiwanda kimoja tu katika nchi ambacho ndiyo kinaingiza nyavu kwa wavuvi, lakini Waheshimiwa Wabunge wakafika hatua ya kusema tumezuia uingizaji wa nyavu.

Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako tukufu hili, Wizara yetu haijazuia hata kidogo uingizaji wa nyavu nchini isipokuwa lazima tukubaliane kazi tuliyoifanya ya kuondoa zile nyavu ambazo zinasemwa na sheria kwamba ni nyavu haramu ni kubwa mno. Ukitazama anayeathirika ni yule mvuvi wa chini kule, tulipokwenda kuzichoma na kuziteketeza kwa mujibu wa sheria, waathirika wakubwa ni wale wavuvi wetu wa kule chini. Mara zote Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakiuliza kwa nini Serikali inajielekeza zaidi kwenda kushughulika na wavuvi wale wa kule chini hawashughuliki na wazalishaji na wasambazaji.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia maoni hayo ya Waheshimiwa Wabunge ndiyo maana sisi hatukukubali kwanza moja kwa moja kufungua mipaka yetu kuziingiza nyavu zile. Tulisema ni lazima turatibu zoezi hili ili tusiende kurudia makosa yale yale kila siku ya kwenda kumchomea mvuvi wetu, mvuvi mnyonge kwa sababu sisi tunaamini sekta hii ya mifugo na uvuvi haiwezi kuwepo bila ya kuwepo kwa hawa wavuvi wetu. Kwa hiyo, nataka niwahakikishieni baada ya kukubaliana na kufanya tathmini hii tutakuwa tuko tayari hata kufungua.

Mheshimiwa Spika, niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba nyavu hizi nyingi zinazalishwa katika nchi jirani mojawapo ambayo haina hata ziwa lenyewe. Sisi hapa hiki kiwanda kinachosemwa cha hapo Arusha tumekipa kweli leseni baada ya kutuomba. Mimi mwenyewe kama Naibu Waziri nimekipitia kiwanda hiki, kina marobota ya nyavu za kuvulia dagaa mengi sana hayana mnunuzi. Tumeelewa concern ya Wabunge ya kwamba inawezekana wale mabwana nyavu zao hazina ubora. Tumekubaliana na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara wanaohusika na masuala ya ubora tuweze kwenda kuhakikisha kwamba nyavu zile zinakwenda kuzalishwa zenye ubora zaidi.

Waheshimiwa Wabunge tunaomba mtuamini ya kwamba jambo hili tunalizingatia ili kusudi sekta yetu ya uvuvi na wavuvi wetu wasiweze kuweza kwenda kuharibikiwa.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna contradictions za sheria ambazo zimejadiliwa hapa na baadhi ya wavuvi wenzangu kwamba sasa inakuwaje juu ya hizi nyavu za dagaa lakini wakati huo huo zinakwenda na zinakamatwa tena. Unafahamu wavuvi nao vilevile ni binadamu na ni wajanja, kule Kanda ya Ziwa kuna uvuvi maarufu unaitwa gizagiza. Zilezile nyavu za dagaa kwa mujibu wa sheria na utaratibu wetu zile huenda kuvua kwa kutumia karabai, lakini watu wamezigeuza, hawatumii tena karabai wamefungia zile karabai zao, usiku wanakwenda kuvua bila ya zile karabai. Wanapokwenda kuvua bila ya zile karabai ndiyo wanaita gizagiza.

Sasa wakati ule wanapokuwa hawatumii karabai wanampata sangara mchanga, wanapata sato na mazao mengine ya uvuvi, ukitumia karabai haupati matatizo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya ufinyu wa muda, naomba niende katika upigaji chapa. Waheshimiwa Wabunge wengi sana wameeleza juu ya upigaji chapa na tena babu yangu Mzee Ndassa pale ameenda na kuniambia mimi kwamba tena wewe Ulega mwenyewe hata hii shughuli ya ufugaji hujawahi kuifanya.

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishieni Waheshimiwa Wabunge mawazo na ushauri wenu wote mlioutoa katika kulinda sekta ya ngozi kwenye eneo hili la upigaji chapa tumeyachukua na sasa timu yetu inafanya tathmini. Kwa sababu hili eneo ni endelevu kwa maana ya kwamba upigaji chapa si kitu cha kusema kwamba kinaisha leo au kesho, ni kitu ambacho kipo kwa mujibu wa Sheria ya Utambuzi wa Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kile ambacho ninyi mmekiomba ni kuhakikisha kwamba tunaboresha, tumeyachukua yale mawazo kwamba tusichome tena ng’ombe badala yake tuwavalishe hereni ama tutafute mbinu nyingine zozote ambazo zitakwenda kuifanya ngozi yetu na mifugo yetu iendelee kuwa na thamani. Mimi nataka niwahakikishieni kwamba jambo mlilotushauri ni jema na tumelichukua na tunakwenda kulifanyia kazi mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, imezungumzwa pia vilevile hoja na jirani yangu Mheshimiwa Dau iliyohusu MPRU kwa maana ya hifadhi ya bahari. Nataka nimhakikishie kwamba kama nilivyokuwa nikijibu kila mara kwamba hifadhi ya bahari ipo kwa mujibu wa sheria lakini yeye concern yake ni juu ya mapato na amezungumzia kwamba kwa nini tusichukue MPRU kwa maana ya Hifadhi wachukue asilimia 50 na Halmashauri wachukue asilimia 50. Kwa sasa hivi asilimia 30 zinakwenda katika Halmashauri ya Wilaya ya Mafia kwa maana ya 10 zinakwenda katika Halmashauri yenyewe na 20 inakwenda katika vijiji ambavyo vimezungukwa na ile hifadhi ya bahari. Ushauri wake wote aliotupatia wa kwamba tunataka twende katika usawa tunauchukua. Haya ni mambo ambayo tuna uwezo wa kuyazungumza, tukakaa kwa pamoja, tukashauriana na kuona ni namna gani bora zaidi ya kuweza kuwasaidia watu wetu.

Mheshimiwa Spika, mwisho nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wengi waliozungumzia ufugaji wa kuku kwamba Wizara yetu inao mradi mkubwa sana wa kuhamasisha ufugaji wa kuku. Kwa hivi sasa tumeshazifikia halmashauri 20 katika nchi nzima. Tunagawa bure kabisa mbegu ambazo ni za Kitanzania zenye kuhimili matatizo na ugonjwa kama vile ugonjwa wa mdondo na mengineo.

Kwa kusema ukweli tutahakikisha kwamba tunafikia Halmasharuri zote nchini. Mradi huu umefadhiliwa na wenzetu wa Bill & Melinda Gates ambapo tunahakikisha mpaka kufika mwaka 2019, Halmashauri zetu nyingi ziwe zimepata mradi huu wa ufugaji wa kuku. Nia na madhumuni yetu ni kuhakikisha tunainua kipato cha wafugaji wetu lakini pia tuwe na uhakika wa chakula vilevile.

Mheshimiwa Spika, yapo magonjwa ya mifugo vilevile yamezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi. Nataka niwahakikishie kwamba sisi katika Wizara tumeweka mkakati madhubuti kabisa wa kupambana na magonjwa ya mifugo. Tumeweka magonjwa ya kipaumbele, yapo magonjwa kama kumi ambayo tumeona kwamba haya tuyafanye kuwa magonjwa ya kipaumbele katika ng’ombe kwa mfano ugonjwa wa kuangusha mimba na magonjwa ya miguu na midomo na katika kuku magonjwa kama vile ya mdondo, yote tumeyapa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi maabara yetu ya pale Temeke Veterinary tuna chanjo takribani nne. Tunaamini kabla ya mwaka huu haujaisha tutakuwa tumeipata chanjo ya ugonjwa unaowasumbua ng’ombe wetu wengi sana, chanjo ya ugonjwa wa homa ya mapafu. Mpaka mwisho wa mwaka huu tunahakikisha kwamba tumeipata chanjo ile. Baada ya hapo ni lazima niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwamba kama tunataka kweli kabisa sekta yetu ya mifugo isonge mbele ni lazima upigaji wa chanjo yaani uchanjaji wa mifugo yetu uwe wa lazima ili kuweza kuifanya sekta hii iweze kukua vizuri na hatimaye tuweze kushindana katika masoko ya kimataifa, tuuze nyama yetu na watu waikubali nyama yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba sana Waheshimiwa Wabunge tutakapofika katika hatua za namna hii nanyi muendelee kutuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya, naomba tena nichukue fursa hii kusema kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia moa moja kabisa. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge yale yote ambayo leo mmetuambia katika Bunge hili na kututaka tuweze kurekebisha ili hali iweze kuwa nzuri zaidi katika sekta zetu hizi za mifugo na uvuvi, tumeyachukua na tunakwenda kuyafanyia kazi. Ninaamini kwamba baada ya muda mfupi mtakuja hapa kutushangilia kwa namna ambavyo tumefanya vyema katika kazi mliyotutuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsanteni sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote na mimi naomba nichukue fursa hii kumshukuru kwanza Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kuweza kushiriki vyema katika shughuli hii ya bajeti ya Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi. Pili, nikushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuzungumza hapa na tatu, kwa namna ya kipekee kabisa, nimpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuhakikisha kuwa wakati wote anaendelea kutusimamia na kuhakikisha kuwa nchi yetu inasonga mbele kwa yale yaliyokusudiwa katika Taifa letu ya kuwaletea maendeleo Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maelekezo mazuri anayotupatia wakati wote na kutusimamia katika kuhakikisha tunamsaidia vyema Mheshimiwa Rais wetu. Kwa namna ya kipekee pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri wangu Luhaga Joelson Mpina, Makatibu Wakuu wetu wote wawili wa Mifugo na Uvuvi Profesa Elisante Ole Gabriel na Dkt Rashid Tamatamah kwa namna tunavyoshirikiana na watendaji wote pale Wizarani katika kusukuma mbele gurudumu hili la Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi ambayo ni Wizara yenye tija kubwa na inayogusa Watanzania walio wengi na hapa leo Waheshimiwa Wabunge wamethibitisha jambo hilo pia.

Mheshimiwa Spika, pia niendelee kuwashukuru Kamati yetu ya Bunge na Wabunge wote waliochangia katika hoja hii inayotuhusu ya Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi kwa sababu tumepata wachangiaji wengi sana. Hii imetupa moyo mpana sana na kwa niaba ya Waziri wangu ni lazima nitoe shukrani kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwa sababu hatukuamini kwamba tungeweza kupata wachangiaji wa namna hii wa kutushauri na kutuelekeza pia vile vile ya namna bora zaidi ya kwenda mbele hatimaye kuyapata matokeo tarajiwa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijielekeze katika hoja. Hoja zimesemwa nyingi sana na Waheshimiwa Wabunge katika upande wa Mifugo, lakini vilevile katika kupande wa Uvuvi. Nijielekeze kidogo katika upande wa Uvuvi; jana katika miongoni mwa wachangiaji waliochangia na mmoja leo amerudia kuonesha kuwa katika kipindi chote tulichohudumu Serikali ya Awamu ya Tano, haijafanya jambo lolote katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi katika sekta hii ya Uvuvi.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba watembee kifua mbele, yako mambo ya msingi tuliyoyafanya na mimi ninayo Ilani ya Uchaguzi hapa na nitaeleza baadhi ya mambo ambayo Serikali ya Awamu ya Tano imeyafanya. Wabunge waliopata nafasi na kusema kwamba hakuna kilichofanyika, kwanza nianze na ibara hii ya 27 ya Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, eneo la (p); kuendelea kupambana na uvuvi haramu ili uvuvi uwe endelevu na wenye tija. Jambo hili Waheshimiwa Wabunge wengi wanaweza kuwa wasijue kuwa limeandikwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, Chama cha Mapinduzi kinataka samaki tulionao leo tuendelee kuwa nao kesho na hata vizazi vyetu vikute samaki hawa na ndiyo maana kikaelekeza Serikali yake kwamba tulinde rasilimali zetu hizi. Sisi tumeifanya kazi hii kama ni kazi ya kipaumbele katika kulinda rasilimali za nchi yetu ziinufaishe nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nataka nikuhakikishie wewe mwenyewe na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote, jambo hili limeleta tija kubwa sana. Uvuvi haramu kwa upande wa bahari ya hindi ulikuwa umekithiri, ulikuwa ni uvuvi wa mabomu, leo katika upande wa bahari ya hindi hauwezi kusikia bomu linapigwa kuanzia Tanga MOA, hadi Mtwara kule Msanga Mkuu hakuna bomu linalopigwa. Tumedhibiti kwa zaidi ya asilimia 99, hakuna bomu linalopigwa na Watanzania wa upande wa huko pwani wameanza kusahau habari ya bomu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya ni mafanikio makubwa bomu liliua watu, bomu lilitishia hata usalama wa baadhi ya miundombinu yetu ikiwemo hata bomba letu la gesi linalotoka Songosongo kuja Somanga kwa ajili ya gesi inayoenda kuzalisha umeme pale Kinyerezi, sisi tumeweza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine mmoja kati ya wachangiaji jana alikuwa anazungumzia juu ya ujenzi wa bandari ya uvuvi. Katika kazi tuliyoifanya kipindi hiki ni kufufua shirika letu la TAFICO, hii ni hesabu nyepesi sana tu. Tumenunua ndege, tusingeenda kununua ndege, isipokuwa kwanza tuwe na shirika imara la kuzisimamia zile ndege, ndiyo maana tukaimarisha ATC, hatuwezi kwenda kununua meli, nani atakayezisimamia zile meli, ndiyo maana tukasema ni lazima tufufue TAFICO. Ufufuaji wa TAFICO ndiyo utakaokwenda kusimamia zile meli tunazozitegemea kuzinunua.

Mheshimiwa Spika, nataka niwapeni habari njema TAFICO imefufuka tena mwanamama mmoja mahiri tumempa kazi ya kuhakikisha TAFICO inafanya vyema. Tumetambua mali zote za TAFICO na TAFICO sasa ipo na imeanza kazi na tayari tuna uhakika wa kupata takriban kiasi cha shilingi bilioni nne kununua meli, meli ambazo zitafanya kazi ya kuvua katika maji yetu ya ndani kwanza, tunafanya hivyo kwa nini?

Mheshimiwa Spika, tunafanya kwa sababu tunataka tuioneshe dunia kwamba tunazo rasilimali, tuwavute wawekezaji, watu walikata tama, hawawezi kuamini kwamba hapa katika maji yetu sisi wako samaki, mwekezaji wa kuweka kiwanda au mwekezaji wa kuleta meli haji tu bila ya kuwa na uhakika wa kuweza kufanya investment ile ambayo anaweza kwenda kuifanya pale.

Mheshimiwa Spika, sisi tumetengeneza mkakati na hivi leo TAFICO inatengeneza business plan ya kisasa ambayo itakwenda kuhakikisha kuwa inaingia hata mikataba. Tunao Wakorea, wameonesha nia ya kushirikiana na TAFICO na tutakwenda kujenga bandari ya uvuvi. Hao Wajapan pia vile vile wameonesha nia ya kushirikiana na TAFICO ambayo itaenda kutuletea tija katika shughuli hizi za uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Ilani pia ya Uchaguzi imetuelekeza juu ya kuhakikisha kuwa tunalinda matumbawe yetu, maeneo ya mazalia ya samaki kwa upande wa kule pwani, hili tumefanikiwa. Kwa nini tumefanikiwa? Upande wa kule pwani tumedhibiti, watu wa Kilwa hapa kama wapo wananisikia na watahakikisha kwamba jambo hili ni la ukweli wa kiasi gani. Pale Kilwa tumedhibiti miamba yetu. Pweza walikuwa wakipatikana kwa uchache sana, pweza ni biashara ambayo inauzwa ndani, lakini tuna-export pia vile vile kwa kupitia mradi maarufu wa SWIOFISH, tumefanikiwa kudhibiti na sasa wanapata mazao ya kutosha watu wa kule pwani kwa ajili ya kuweza kuinua maisha yao, hiyo ni kazi yetu sisi.

Mheshimiwa Spika, Ilani imetuelekeza pia vile vile tutengeneze matumbawe yasiyokuwa ya asili ambayo tumeyatengeneza pale Bagamoyo na kule Nungwi, tumepeleka ya kutosha, hizi zote ni kazi tulizozifanya.

Mheshimiwa Spika, Ilani katika eneo (d) linatuelekeza sisi kuimarisha Masoko yetu ya Feri na kuimarisha Masoko yetu ya Kirumba. Katika jambo tulilofanikiwa ni hilo, tumeimarisha Soko letu la Feri na tumeimarisha Soko letu la Kirumba. Kirumba kabla sisi hatujaingia katika kupewa dhamana hii na Mheshimiwa Rais, nataka niwahakikishie ni eneo ambalo lilikuwa linakwenda vizuri, lakini sivyo kama tunavyokwenda hivi leo. Kirumba sasa inakusanya kwa mwezi mmoja milioni 600, eneo ambalo tulikuwa tunakusanya milioni 30; kutoka milioni 30 mpaka milioni 600 kwa mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hi kuwashukuru na kuwapongeza sana watendaji wote, Mheshimiwa Mbunge wa Ilemela Dkt. Angelina Mabula na wengine wote pale Mwanza kwa namna walivyotuunga mkono katika kuhakikisha Soko la Kirumba linafanya vizuri. Soko la Kirumba limetengenezewa mzani wa kisasa, unapima mazao yetu yote yanayoingia pale. Tulikuwa tunapoteza pesa nyingi sana kama Serikali, hivi leo tunafanya vizuri. Pale feri tunafanya ukarabati mkubwa sana, tunapeleka zaidi ya bilioni 1.5 pale kulifanya Soko la Feri liwe soko la kisasa, nani anasema Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi haijatekelezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nilimtaka awepo hapa ili nimwoneshe kwa namna gani, kazi kubwa tuliyoifanya. Wabunge wa Chama cha Mapinduzi litakapokuja suala la Uvuvi, nawaomba watembee kifua mbele, Serikali ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli imefanya kazi kubwa na itaendelea kufanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wa mifugo, nataka nikuhakikishie kwamba tumefanya kazi kubwa. Jambo moja amelisema jana Mheshimiwa Mbunge Jackline Msongozi, naomba niende na hilo tu, mwaka 2016/2017, wakati Mheshimiwa Rais anakwenda kutembelea pale Tanga alipita katika Kiwanda cha Tanga Fresh akaona liko tatizo la ardhi na mtaji wao ni mdogo, akawawezesha. Wale watu wa Tanga Fresh hawakuwa wanazalisha maziwa ya long life, hivi leo wanazalisha maziwa ya long life, tunajivunia, hata maziwa ya kutoka nje yasipokuwepo Tanga Fresh na ASAS wote tumewawezesha sisi. ASAS wamewezeshwa kupitia ubunifu, ubunifu uliofanywa na Waziri wangu Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina, tumeanzisha dawati la sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, dawati la sekta binafsi tumelizindua sisi wenyewe mwaka jana mwezi wa 10, limeleta tija kubwa, limesaidia viwanda vya nchi hii, limesaidia wavuvi wa nchi hii, tuna ushirika leo. Ushirika unajibu Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, ushirika pale Kikumba Itare tumewapelekea milioni tano, nimekwenda kukabidhi mimi mwenyewe. Pale Igombe, Mwanza tunawapelekea milioni tano, anakwenda kukabidhi Mheshimiwa Waziri. Tumepeleka kila mahali, tunainua ushirika na kama haitoshi tumepeleka hata pembezoni ambako wanakwenda kufanya mabwawa, pale Peramiho kwa Mheshimiwa Jenista tumekwenda kuwasaidia waweze kuanzisha mabwawa ya ufugaji wa samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeanzisha Chama Kikuu cha Ushirika katika nchi ambacho kinawaunganisha wavuvi wote kwa lengo na nia tuwakopeshe zana za uvuvi, tuwasaidie wakopeshwe pesa na mabenki waweze kupata tija ya kazi yao wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote kazi inaendelea na sisi hatutakata tamaa katika kuhakikisha kazi hii tuliyopewa ya kulisogeza Taifa letu mbele, ya kumuunga mkono Mheshimiwa Rais, hatutarudi nyuma, tutaendelea kusonga mbele, upungufu ule mliotueleza sisi kama wanadamu tutaufanyia kazi katika kuhakikisha kuwa Taifa letu linasonga mbele katika rasilimali zake hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa muda huu wa kuweza kuchangia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba awali ya yote nianze kwanza kwa kutoa shukrani zangu za dhati sana kwako kwa fursa hii ambayo umenipatia, lakini nitoe pia shukrani kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango mizuri sana na mikubwa mliyotupatia ya fikra na mawazo chanya kwa ajili ya kuweza kupeleka mbele sekta zetu hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwa namna ya kipekee nimshukuru sana Waziri wangu, Mheshimiwa Mashimba Ndaki na Makatibu Wakuu wote wawili pamoja na wataalam wetu na Wakuu wa Taasisi na Idara mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa shukrani hizi nitoe pongezi nyingi pia kwa Wabunge kwa namna ambavyo wametupa michango yenye kujenga sana, wakiongozwa na wewe mwenyewe ambaye kiasili ni mfugaji, tunakushukuru sana na tuna hakika kwamba michango yenu hii tunakwenda kuifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa uchache wa muda ninaomba nijielekeze katika kujibu hoja kadhaa za Waheshimiwa Wabunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nitaanza na upande wa mifugo na naomba niseme juu ya mipango yetu ya kibajeti kama ambavyo inasomeka katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge walio wengi wameeleza wazi juu ya kutokuridhika kwao kwa namna ambavyo nchi yetu ina mifugo mingi sana, lakini bahati mbaya sana mifugo hii kutokuwa na mchango mkubwa kwenye pato la Taifa na katika pato la mwananchi mmoja mmoja.

Mheshimiwa Spika, Serikali tumeliona jambo hili, jambo hili linatufanya sisi kama wauzaji wa mifugo tusifanikiwe sana kwa maana suppliers na demand (mahitaji) ni makubwa sana. Kwa hiyo sisi Watanzania wote tunaowajibu wa kuhakikisha tunalichukua kama fursa jambo hili. Na nini ambacho tumejipanga nacho ili sisi Watanzania tuweze kuitumia vyema hii advantage ya kuwa ni suppliers wa mifugo tena duniani.

Mheshimiwa Spika, moja ya jambo kubwa linalotusumbua kwa kipindi kirefu, mifugo haina insurance, ni perishable good, jambo hili limetufanya hata bankers wasiwe na appetite ya kuweza kuingiza pesa katika shughuli za mifugo. Leo hii tunakwenda kwa mfano katika Eid, wakati wa Eid biashara nyingi sana ya mifugo inafanyika, jamii ya Kituruki peke yake inanunua na kuchinja ng’ombe wasiopungua 15,000, jamii moja tu hiyo, lakini utatazama namna biashara ile inavyokwenda.

Mheshimiwa Spika, ukiitazama biashara ile inavyokwenda yule mnunuzi anataka awe supplied wale ng’ombe na akishakuwa supplied wale ng’ombe ndiyo sasa baada ya wiki moja hadi mbili aweze kulipa. Jambo hili linawafanya watu wetu wasifanikiwe kwa sababu hawana cash na wanapokwenda benki hawawezi kupata hii pesa kwa sababu tu mifugo as a perishable good, haikubaliki katika kupewa pesa.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumefika hatma ya jambo hilo, NIC wanaenda sasa kutupa uhakika wa kuwa na bima ya mifugo ambayo itawafanya wafugaji wetu wawe na uhakika wa kwenda kukopesha katika miaka minne hii TADB Benki yetu ya Kilimo imeweza kupata application za mikopo ya shilingi bilioni 85, mikopo pekee waliyoitoa katika miaka minne hii ni shilingi bilioni 26. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kweli tunataka twende mbele ni lazima tutoke mahala huko, lakini kama haitoshi moja ya mkakati ambao wameusoma Waziri hapa ni kuhakikisha kwamba tunaboresha kosafu zetu, kwa nini kosafu zetu, tunahitaji kuwa na quality ya ng’ombe, tunahitaji kuwa na quantity ya uhakika, tunahitaji kuwa na constant supply ya ng’ombe. Kwa sababu leo tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri alishiriki kikao cha Mheshimiwa Rais pale Ikulu, Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, watu wapo tayari kununua ng’ombe wetu, lakini leo hii mtu mmoja akiambiwa apeleke constant supply ya tani saba kila mwezi hapa tutatafutana, ni kwa sababu ya constrain ya kuwa na kosafu na mipangilio yetu haijakaa sawasawa. Wizara imejipanga vyema katika risala hii utaona tumeweka pesa zaidi ya milioni 600 kwa ajili ya kufanya massive artificial insemination, tunakwenda katika Halmashauri zote zenye mifugo na kuhakikisha kwamba hatuishii kuwapandisha tu, lakini kuna gharama kubwa ya kuwaweka kwenye heat. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wale ng’ombe jambo linalowasabisha wafugaji wengi washindwe ni kukaweka kwenye heat, tunataka tuwapeleke kwenye heat synchronization kwa makundi, tutakuja Kongwa, tutakwenda Kiteto, tutakwenda Monduli, tutakwenda Longido, tutakwenda kote kwa wafugaji na kule kwa Dkt. Chaya alipopasema ambapo ni Manyoni. Tukiyafanya haya ya kupata massive artificial insemination tutapata kosafu zetu na baada ya muda tutaanza ku-realize juu ya kuwa na ng’ombe walio bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, biashara ya unenepeshaji ng’ombe ni biashara ya uhakika sana, ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wakati tunaendelea kuhamasisha jambo hili sisi wenyewe pia vilevile tuwe ni mfano mzuri sana, ni utajiri wa wazi ambao mimi ningeomba sana Wabunge wengi tuingie, leo unamnunua ng’ombe ana kilo 150 ambaye huyu ukimchinja carcass weight yake ni nusu maana yake kilo 75, ukimpeleka sokoni hakubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ng’ombe huyo ukienda katika project ya kunenepesha maana yake ni siku 90; kwa hii breed yetu ni nusu kilo kwa kila siku, lakini kwa breed ya boran ni kilo moja kwa kila siku, kwa hivyo huyu ukimpa siku zako 90, huyu ng’ombe anakwenda kuwa na kilo zaidi ya 150 kwa hiyo atakuwa na kilo takribani 240 mpaka kilo 300 ambayo akipata carcass weight anapata kilo 150 hadi 200 na ukimpeleka sokoni anauzika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeeleza hili, ili kuwapa Waheshimiwa Wabunge matumaini na namna ambavyo Wizara yetu ilivyojipanga hiyo ni sambamba na kwenda kutatua kero kubwa inayotusumbua kwa muda mrefu ya gharama za flight na Serikali kupitia Wizara yetu ya Ujenzi na Uchukuzi, umeona tumejipanga vyema eneo hili katika kuhakikisha kwamba…

(Hapa kengele ya kwanza ililia)

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nasikia kengele hiyo.

SPIKA: Bado dakika tano

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ujenzi imeandaa kununua ndege mwaka huu ndege ya cargo itakayobeba a straight destination, kwa hiyo hapa tutachukua nyama zetu zitakwenda Jeddah, zitakwenda Oman, zitakwenda wapi moja kwa moja, kwa hivyo hii ni fursa kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia vilevile tulikuwa na tatizo kubwa la delay pale katika bandari yetu ya Dar es Salaam kwa sababu mizigo yetu hii ikienda inakaa kwa muda mrefu. Wizara ya Ujenzi imejitahidi, naomba tusikate tamaa, tunawaombeni kwa heshima kubwa tupitishieni bajeti yetu, mipango ya Serikali tuliyonayo ni mikubwa ya kuhakikisha sekta hii inakuwa ili kusudi sasa iweze kuchangia vyema katika pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie sasa kwa upande wa uvuvi; uchumi wa blue; uchumi wa blue umesemwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi katika risala ya Mheshimiwa Rais ameeleza vizuri sana, tutanunua meli, meli nne Zanzibar, meli nne Bara na katika mwaka huu 2021/2022 tunaanza nalo jambo hili.

Waheshimiwa Wabunge wengi wa Zanzibar walitaka kujua jambo hili linafanyika Bara tu au linafanyika na Zanzibar tunafanya kwote kuwili hapa bara tunanua meli mbili na kule Zanzibar tunanunua meli mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tena tuna pesa za kutosha za kuhamasisha ufugaji wa samaki katika Ukanda wa Pwani, tunazaidi ya shilingi bilioni 15 zinazokwenda kufanya kazi hii, hii ni pamoja na mwani, hii ni pamoja na kaa unenepeshaji, hii ni pamoja na majongoo bahari, hii ni pamoja na kazi zingine zote zitakazowasaidia vijana sio tu Bara tunakwenda mpaka Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge tunawaombeni sana mjipange katika mkao ule wa vyama vya ushirika na vikundi vya vijana hawa ili tuweze kuitumia vyema hii fursa. Nataka niwahahakishie kwamba jambo hili lipo tayari na tumejipanga nalo vyema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi katika kuhakikisha kwamba tunaongeza productivity kule baharini, tunacho kitu tunaita FADS yaani Fish Aggregative Devices, hii tunakwenda kuweka kule katika bahari, tunazo hizi ni takribani tisini zitaenea katika ukanda wote ule wa Pwani, hii nia yake ni kuwavuta wale samaki.

Mheshimiwa Spika, mmoja katika Waheshimiwa hapa, Mheshimiwa Asya Mwadini alisema kwamba samaki sasa wanakosa maeneo ya kuzaliana. Tumeliona jambo hili na sayansi yake ndiyo tunakwenda kuweka zile fish aggregative devices kuanzia Moa mpaka kule Mtambaswala zitaenea hizi, hizi nia yake nikuongeza mazalia ya samaki, hilo jambo tayari tunalo tupitishieni huu mpango ili tuhakikishe kwamba tunakwenda kuyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi, jambo lingine zuri tunalokwenda kulifanya ni kuanzisha vichanja vya samaki; ukanda wote huo utapata vichanja vya kukaushia dagaa wetu, hatutaki kuona dagaa wanaoza, hatutaki kuona samaki wanaoza, hii ni rasilimali ya Taifa letu, tunataka tuone watu wanaendelea ku-export na nimewasikia Wabunge wengi wanazungumzia juu suala la kuhakikisha kwamba wale foreigners wanaokuja kununua, sisi wenyewe ndiyo tuwawezeshe watu wetu wazawa ili waweze kununua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kwa sababu ya muda naomba nimalizie kwa kuwaeleza na kuwapa matumaini Waheshimiwa Wabunge wote, Serikali yetu imejipanga vyema katika hii blue economy na pesa za kununua meli zimeandaliwa, zipo tayari kwa maana mradi huo upo, ujenzi wa bandari hili lipo tayari pia vilevile na tunashirikiana vyema sana, kwa maana ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya Bara, lakini na Wizara yetu kwa upande wa kule Tanzania Visiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa kwa umuhimu, katika kujibu changamoto inayowapata wafugaji wengi tunakuja na teknolojia mpya ya malisho inaitwa JUNCAO, hii imeonesha mafanikio makubwa duniani. Ndugu zetu wa China tunaendelea nao na majadiliano.

Mheshimiwa Spika, hii itakwenda kujibu hata yale maeneo ya Longido, Monduli, Kiteto yenye kuonesha ile hali ya ukame na kwako Kongwa tunataka tufanye ni sehemu ya kwanza kabisa ya kwenda kupanda hii JUNCAO na hii JUNCAO itaenda kuondoa ile Kongwa wheats inayoonekana pale kama maua meupe hivi, lakini kumbe ni mtihani ule. (Makofi)

Nataka nikuhakikishie ng’ombe akiiona JUNCAO anaikimbilia yeye mwenyewe, tumejipanga kuhakikisha tunashirikiana na wenzetu watafiti na wengineo ili kuleta teknolojia hii itakayokwenda kujibu kilio cha malisho cha wafugaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, nakushukuru sana, waarabu wanapenda sana wale mbuzi wadogo wadogo wa Masai breed, nawaombeni sana Waheshimiwa Wabunge tunaleta kopa ng’ombe, lipa ng’ombe, kopa mbuzi, lipa mbuzi, nendeni mkahamasishe tuhakikishe kwamba wanataka wale mbuzi wa kilo saba mpaka kilo nane, hawataki mambuzi yaliyokomaa sana. Tafadhalini sana hii ni fursa tunataka tuwatoe Watanzania katika umaskini na tuweze kupandisha pato la Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri Abdallah Ulega, tunakushukuru sana kwa ufafanuzi ambao umeutoa na kwa matumaini ambayo tumetupatia Watanzania, umesema neno moja kunenepesha kaa. Kaa ananenepeshwa?

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana tena kwa fursa hii, biashara ya kaa fattening inaitwa kaa, sorry crab fattening kwa maana ya kwamba yule kaa tunachukua wakiwa wadogo wadogo kutoka kule baharini, kwa sisi watu wa kule Ukanda wa Pwani tunafahamu jambo hili. Kwa hiyo, wale wanaokotwa, tena unaokota, kwa muda mrefu sasa sisi watu watu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumekuwa tukikimbizana na Watanzania wanaotumia fursa ya kuwauzia Wachina wanahitaji sana tena wanahitaji sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa sisi tumeona kwa nini tukimbizane nao, tuwatengenezee utaratibu uliokuwa mzuri, watu wafundishwe, waokote wale kaa wakiwa wadogo wadogo, watengeneze majaruba kule pwani, wakishatengeneza yale majaruba, wanakula, tena wale ulaji wao huwawekei chakula chochote ni yale yale maji, law types na high types maji yakiingia na kukupwa tayari wewe unakuwa umenenepesha na unauza unapata pesa nyingi sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma na mwingi wa ukarimu kwa kupata fursa kusimama mbele ya Bunge hili Tukufu na kutoa mchango wangu katika hoja hii.

Mheshimiwa Spika, baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu naomba pia niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani yake kwangu ya kunipa nafasi kuhudumu kama Waziri wa Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba nimshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa na pia naomba nichukue fursa hii kukushukuru wewe binafsi, Naibu Spika na Wenyeviti wa Bunge kwa uwezo na umahiri mkubwa mnaoonyesha katika kuliendesha Bunge letu.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nimshukuru Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Comrade Mheshimiwa David Ernest Silinde kwa kunipa ushirikiano katika kutekeleza majukumu ya Wizara. Pia napenda kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliopata nafasi ya kuchangia kwenye bajeti hii, bajeti ya protein, bajeti ambayo imepata wachangiaji wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa hoja zilizowasilishwa hapa na kuchangiwa kwa vyema sana na michango mizuri sana ya kina yenye lengo la kuboresha utekelezaji wa majukumu ya Wizara yangu.

Mheshimiwa Spika, mifugo na uvuvi ni utajiri. Kupitia michango mingi iliyotolewa na Wabunge, takribani Wabunge 54 waliochangia kwa maneno ya kuzungumza Bungeni na wachache waliochangia kwa kuandika inathibitisha juu ya ukubwa na umuhimu wa Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha katika michango hiyo imedhihirika wazi umuhimu wa kuimarisha Wizara kupitia sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali inayoongoza Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Sekta ya Uvuvi pia imepanga kutekeleza vipaumbele vinavyoendana na kufungamanisha uchumi wa buluu kwa kuhakikisha kuwa rasilimali za uvuvi zinasimamiwa ipasavyo ili kuwa na uvuvi na ukuzaji viumbemaji endelevu, maendeleo ya viwanda, ukuaji wa kipato cha mtu mmoja mmoja na Pato la Taifa kwa ujumla kwenye maji baridi na maji chumvi na kukabiliana na changamoto ya upungufu wa watumishi katika ngazi ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mifugo ni dhahiri kuwa masuala ya kuendeleza malisho, ajira kwa vijana, mauzo nje ya nchi, utafiti wa mifugo ikiwa ni pamoja na kuendeleza kosafu bora za mifugo ni ya umuhimu katika kuongeza tija katika uzalishaji wa maziwa na nyama, mayai na ngozi, kuendana na mnyororo wa thamani na uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, napenda kuwatambua Waheshimiwa Wabunge wote waliotoa hoja mbalimbali kuhusu Wizara ambapo jumla ya Wabunge 54 kama nilivyokwisha kusema wametoa michango yao. Kuna waliotoa maoni yao kwa kuzungumza hapa Bungeni na wengine kwa maandishi. Naomba sasa wote hao niwatambue kama ambavyo watakavyokuwa wamesomwa katika risala yangu.

Mheshimiwa Spika, michango ya Waheshimiwa Wabunge niliowataja katika risala ilikuwa ni mizuri sana na iliyosheheni busara, hekima na changamoto. Aidha siyo rahisii kujibu kwa kina na kutosheleza hoja zote za Waheshimiwa Wabunge kwa muda huu mfupi nilionao hapa katika membari hii. Ninaahidi kwamba hoja zote tutazijibu kwa maandishi na kuwapatia Waheshimiwa Wabunge wote.

Mheshimiwa Spika, ushauri na maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo umezingatiwa. Hata hivyo ningependa nitumie muda mfupi nilionao kujaribu kutoa ufafanuzi katika baadhi ya hoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ziko hoja mahususi kadhaa zilizozungumzwa hapa. Nikianza na upande wa mifugo. Katika upande wa mifugo iko hoja iliyozungumzwa juu ya hereni. Serikali ilianza kulitekeleza zoezi hili kupitia Wizara ya Mifugo na Uvivu na baada ya utekelezaji iligundulika kwamba yako makosa ambayo tuliyatekeleza kwa wakati ule. Na kwa hekima na busara za viongozi wetu wakaitaka wizara irejee, ifanye tathmini ijiridhishe kama ushirikishwaji umefanywa sawasawa; tuangalie juu ya bei, juu ya ubora wa bidhaa zile.

Mheshimiwa Spika, kazi hii sasa tumekwishakufika mwisho; kwa maana ya kwamba tumepata yale yote ambayo Serikali imeelekeza, kwa maana uongozi wetu umeelekeza maana maelekezo haya yalitolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu katika Bunge hili Tukufu. Baada ya kutoa maelekezo yale Wizara ya Mifugo na Uvuvi ilichukua hatua sawa na maelekezo yale. Na hapa, ingawa kule mbele nitaendelea pia, nataka nieleweshe, maana yupo mmoja katika wachangiaji, Mheshimiwa Luaga Mpina, amezungumza kuwa maelekezo yanayotolewa na viongozi wetu, akiwemo Mheshimiwa Waziri Mkuu, na amemtaja haswa yeye mahususi, kwamba hayafanyiwi kazi. Kufanyiwa kazi kwa jambo hili la hereni, kwa maana ya tathmini na kujiridhisha juu ya bei na juu ya uwezo wa zile hereni zenyewe ni moja ya ushahidi wa kwamba viongozi wanapoelekeza hufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nitakuja hapa kuwaomba Waheshimiwa Wabunge, ya kwamba katika mkakati wetu wa utekelezaji wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, la kwanza kwenye kwenda kuitekeleza sheria hii kwenye bajeti hii tuligundua kwamba tuna jukumu la kuwashirikisha ipasavyo Waheshimiwa Wabunge na wadau wengine wote. Ninawaombeni kwa heshima kubwa na taathima tukubaliane ya kwamba leo tupitishe bajeti hii kisha tuanze engagement kati ya Wizara na ninyi viongozi. N mawazo yenu yote tutayachukua kwenda kuboresha zoezi hili. Nataka niwahakikishie litakwenda kuwa zoezi zuri sana litakalokwenda kuinua uchumi wa wafugaji, uchumi wa Taifa letu na mchango chanya wa hili Taifa. Msiwe na wasiwasi wowote, sisi ni watu wasikivu na ni watu ambao tuko tayari kushirikiana nanyi Wabunge wetu ipasavyo kabisa.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine mahususi ambayo ningependa kuzungumza hapa ni hoja ya malisho. Nimesema katika bajeti ya kwamba tumetenga fedha za kuhakikisha mashamba yanayomilikiwa na Serikali ambayo yaliyojaa nchi nzima na kwa kiasi kikubwa yamekuwa ni mapori, na Waheshimiwa Wabunge mmesema hapa. Nataka niwahakikishieni ya kwamba moja ya jukumu kubwa tutakalokwenda kufanya ni kuyafanya mashamba yale yawe ni mashamba ya uwekezaji na uzalishaji ili yaweze kuwa na tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, tunazo njia mbili kubwa za kufanya, njia ya kwanza ni kwa kutumia fedha zetu wenyewe ambazo tumeziweka katika bajeti na njia ya pili tutafungua milango ya uwekezaji. Nilishasema katika Bunge ikiwa wewe Mbunge, ikiwa unaye mwekezaji yeyote mlete Wizarani atuambie andiko lake, alete business plan yake, alete mpango wake sisi tuko tayari kutoa ushirikiano tuzalishe.

Mheshimiwa Spika, mathalani kule Ruvuma tumechagua ni eneo la uzalishaji wa mahindi aina ya mahindi ya njano (yellow corns). Kwa muda mrefu sasa mifugo kama vile wazalishaji wa kuku wamekuwa wakihangaika; inapofika kipindi cha kiangazi huwa wanapata tabu sana namna ya kupata mahindi. Mimi na wenzangu wizarani tumeshauriana na tumekubaliana mashamba ya upande wa kule tuliyonayo pale Hanga, Ngadinda na kwingineko, Songea kule tunakwenda kuzalisha yellow corns. Yellow corns hii itakwenda kwa ajili ya kutengeneza uhakika wa chakula cha kuku na mifugo mengine. Kwa hivyo niwahakikishieni jambo hili tunakwenda kulifanya; na kwa mara ya kwanza Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumetengeneza mpango wa kwamba sio kwa kutegemea mvua tena, tunakwenda kufanya mechanization tunakwenda kumwagilia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunafikiria kwamba hata nyasi imwagiliwe, sio mahindi tu na mpunga hata nyasi tuzimwagilie, hayo ndio mawazo tuliyonayo. Mmoja katika ya Waheshimiwa Wabunge humu amesema kwamba kwanza tosheleza chakula cha ng’ombe wako hapa nyumbani.; ni ukweli tutatosheleza chakula cha hapa nyumbani. Lakini niwaambie Waheshimiwa Wabunge, sitaki kusema maneno mengi; angalia leo hii chakula cha mifugo inayolishwa kule Asia kwa kiasi kikubwa sana ilikuwa inatoka Sudan na jirani zetu wa Kenya.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, kama hatutaweza kutumia tena fursa hii sisi Watanzania leo haitatokea tena wakati mwingine. Kila mmoja hapa anajua matatizo yanayowapata majirani zetu, hii kwetu sisi ni fursa. Wamekuja, mimi nimempokea hapa Waziri wa Kilimo wa kutoka Saudia nimekaa naye, walikuwa wanachukua nyasi kutoka Sudan, moto unaowaka kule sitaki kusema kwa nguvu sana hapa Bungeni. Hiyo kwetu ni fursa tutapata forex, tutapata fedha za kigeni tutatumia hiyo kama ni ajira ya watu wetu. Kwa hivyo ni ukweli kwamba ng’ombe wetu hapa nyumbani huwa wanahainga. Nilisema, kwamba tunataka tuone gari zinatoka sehemu moja zinakwenda sehemu nyingine zikiwa zimebeba nyasi. Kama vile ambavyo tunatoa mahidni kutoka sehemu moja kupeleka kwa wahitaji na ndivyo hivyo tunataka tufike katika hatua ya kuchukua nyasi kupeleka Kiteto, Simanjiro ili ile mifugo ya kule Lungido iweze kuokolewa. Ndugu zangu inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nilikwenda Simanjiro na Comrade Ole-Sendeka, na nilikwenda Kiteto na rafiki yangu Comrade Olelekaita, niliwashuhudia ng’ombe wakati wa ukame mkali wakinyweshwa uji, yes, ndiyo, kwa ajili ya kutafuta survival. Na sisi binadamu tumekuwa tukijinusuru kwa kupelekeana mahindi ya nafuu. Nasema hivi tunakwenda sasa katika mechanization tutazalisha majani ya kutosha kama tunajihami tutawahami na mifugo yetu pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa jambo la vaccination hapa, kwa maana ya chanjo. Chanjo ni muhimu sana. Ili tuuze ng’ombe wetu vizuri chanjo na herein, kwa maana ya kuitambua mifugo yetu ni jambo la muhimu. Yuko ndugu yangu mmoja pale Mwanza anaitwa Chobo; alikuwa anauza nyama kule UAE; Chobo amekataliwa kuuza nyama Uarabuni hivi sasa, hauzi tena. Kiwanda kiko kizuri sana pale ni kwa sababu ya vitu hivi. Sisi tumedhamiria, kabla hatujakwenda huko nitakaa na Waheshimiwa Wabunge wote, kila mmoja anajua ana hoja yake, kwa nini anasema isiwe hereni, milango yangu iko wazi. Tutahakikisha tunakaa tunakubaliana, tutakwenda na campaigns za uhakika ambazo hazitatuletea taharuki ya namna yoyote.

Mheshimiwa Spika, nataka tutoke katika kuuza tani 12,000. Kwa nini sisi tuzalishe nyama tani 800,000 zinatutosheleza humu nyumbani, kwa nini hatuuzi tani 100,000 nje ya Taifa letu wakati uwezo wa kuuza na masoko yako makubwa sana? Ndugu zangu kupanga ni kuchagua, tunapata tupate forex, tupate ajira za watu wetu, tupate uchumi mkubwa. Yako mambo ni lazima tuyafanye ili kusudi tukubaliane hii mifugo yetu iweze kutunufaisha na inufaishe Taifa letu. Hii GDP inayochangiwa hivi sasa kwa asilimia nane ninawahakikishieni kama kuna nafasi nzuri na rahisi ya kuinua ni katika mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na Mungu Mkubwa sana Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshatutengenezea njia rahisi sana kwa diplomasia kubwa sana ya uchumi. Wanenepeshaji wa ng’ombe, wale wa mbuzi, wale wa kondoo na wengine tukae mkao wa utayari. Nataka niwahakikishieni hatutakwenda katika zoezi lolote baada ya bajeti hapa, tunatengeneza engagement plan na implementation plan ya uhakika. Waheshimiwa Wabunge wote msiwe na wasiwasi. Wale mliokuwa mnakusudia kuchukua shilingi yangu kwenye jambo hili naomba kabisa kwa uhakika wala msiwe na wasiwasi huo, manake tutakaa na mambo yatakuwa mazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya tatu, Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia kuhusiana na wakala, na hii inahusiana na miundombinu ya mifugo kila Mbunge anataka josho, kila Mheshimiwa Mbunge anataka rambo, kisima kirefu cha maji, kila Mbunge angependa awe na bwawa la mifugo na akitazama anaiona bajeti ya Waziri wa Mifugo imetengeza marambo manane tu kwa mwaka. Way forward mmeitoa ninyi wenyewe, mmesema hapa, na nimewasikieni, kuanzia kwenye kamati ya Bunge iliyowasilisha hapa na kuja kwa Mheshimiwa Mbunge mmoja mmoja mmesema hapa. Kwamba Wizara inasimamia miradi kutokea Dodoma. Bwawa linajengwa Kiteto kwa Mheshimiwa Olelekaita, bwawa linajengwa kule Simanjiro, bwawa linajengwa kule Longido, bwawa linajengwa kule Mkuranga ndani Mkurugenzi yuko pale Dodoma peke yake na engineer wayasimamie yale.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamesema, kwamba, hapa tunalo jambo la kufanya, na katika jambo la kufanya mnadhani ya kwamba tutengeneze wakala. Waheshimiwa Wabunge, wafugaji wenzangu nataka niwakumbusheleo hapa, kwa ufupi sana. Watu wa kilimo kupitia Tume ya Umwagiliaji wamepata fedha nyingi sana ninyi, nyote ni mashahidi na mmepitisha nyie wenyewe hapa. Zile schemes za umwagiliaji wakulima watakaokuwa wanatumia watakuwa wanachangia nadhani tunaelewana hapo. Sisi binadamu, nimetoa mifano ya RUWASA, yale maji tunayoyatumia sisi tunachangia. Ninafahamu, ndiyo maana mkasema tupate wakala. Ninawajua wafugaji, nimekaa nao miaka kadhaa sasa, wako tayari kuchangia lakini katika mambo ya uhakika.

Mheshimiwa Spika, hoja hii inatosheleza kuwaambieni ya kwamba tunalichukua jambo hili ndani ya Serikali tunakwenda kulianzishia harakati zake. Tutali-fast track tukipata baraka Inshallah Ta’ala jambo litakuja litapita lita-solve matatizo ya watu wote hapa. Ninyi leo kazi yenu ni nyepesi sana tu, nakuombeni kwa heshima kubwa na taathima tena kwa mara nyingine nipitishieni muone mchakamchaka utakaopigwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niende katika uvuvi; limesemwa jambo kwa mapana na marefu sana hapa juu Lake Tanganyika. Waheshimiwa Wabunge wa Kigoma, Rukwa; narudia tena; limesemwa jambo la Lake Tanganyika kufungwa. Waheshimiwa Wabunge wa Kigoma, Katavi na Rukwa wamesema kwa mapana sana na wananchi wamewasikia, na mimi na wenzangu Serikalini tumewasikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba itifaki hii ilisainiwa ipo ndani ya Serikali, ilikuwa na lengo jema; lakini itifaki hii haikutulazimisha sisi nchi wanachama ya kwamba namna ya utekelezaji wa ile itifaki ufanane, haikuwa hivyo. sisi hapa katika Ziwa Tanganyika tuna kitu kinaitwa kilimia; mmoja miongoni mwa Waheshimiwa Wabunge amesema hapa. Kilimia, najua Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda, Mheshimiwa Aida Khenani, Mheshimiwa Bindyaguze, na Waheshimiwa Wabunge wengine wanafahamu vizuri. Kilimia lile ziwa huwa linajifunga lenyewe automatically, hasa kipindi hiki cha baridi. Nimefurahi kwamba Waheshimiwa Wabunge kutoka mikoa hii mmewaleta wapiga kura, wavuvi wenyewe. Ndugu zangu hakuna sababu yoyote ya kupata taharuki.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge nataka niwahakikishieni, kama ambavyo tumewaandalia mkutano kesho; ninafahamu tuna mkutano na wakuu wa mikoa hiyo yote, Waheshimiwa Wabunge wote, wakuu wa wilaya zote, wakurugenzi wote, kwa kuwa hoja ni ushirikishwaji. Wabunge neno hili la ushirikishwaji tunakwenda kulikamilisha kesho pale St, Gasper, tunakaa tunajadili. Kwa hiyo hakuna hofu, wala hakuna mtu yoyote apate wasiwasi ya kwamba labda kuna jambo linalohusu kufungwa kwa ziwa. Niwahakikishieni, narudia tena, issue si ni kushirikisha? basi nataka niwaambie mimi kwa heshima kubwa na taadhima na wenzangu kule Serikalini, hakuna jambo tunaloliheshimu kama kuwaheshimu watu ninyi mliopigiwa kura na wananchi. Wanasema sauti ya wengi ni sauti ya Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kilumbe na Waheshimiwa wote, Mheshimiwa Bidyanguze, Mheshimiwa Aida, Mheshimiwa Kavejuru, Mheshimiwa Sylivia, Mheshimiwa Ndalichako, Mheshimiwa Kandege, Mheshimiwa Kakoso na Waheshimiwa Wabunge wote niwaondoe hofu. Waambieni wana-Tanganyika wavuvi wa Ziwa Tanganyika waendelee na shughuli zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Daktari Samia Suluhu Hassan kama mnaona jambo kubwa Mheshimiwa Rais wakati wote amekuwa akilisisitiza kwetu sisi wasaidizi wake ni kutokuleta taharuki. Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan Amejenga msingi imara wa zile “R” nne, kila mmoja anazijua hapa. Ikiwa yeye mwenyewe Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefungua milango anakaa na kila mtu, anazungumza naye, anapata kufanya reconciliation hata; yale watu tuliodhani kuwa ni magumu kwa Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan yamekuwa ni mepesi. Sasa mimi Abdallah Ulega ni nani nisijifunze? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hakika nataka niwaondoeni hofu juu ya jambo hili ndugu zangu. Tunazo njia nzuri sana za kuendea mambo, msiwe na wasiwasi na wavuvi msiwe na wasiwasi, wakati wa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni wakati wa uzalishaji, ni wakati wa kukuza uchumi wetu na hakuna sababu nyingine ya kubabaika. Mifugo na uvuvi ni utajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia juu ya mamlaka ya uvuvi ninawaelewa, na Kamati ya Bunge imetuelekeza juu ya jambo hili. Niwakumbushe; katika Sera ya Uvuvi ya Mwaka 2016 jambo hili limetamkwa, na sisi Serikalini tumelichukua. Tumelichukua kwa sababu tumekuwa tukifanya kila mara operations. Ninyi wote hapa mmesema, kila Waziri anayeingia katika Wizara hii anafanya operation. Tunachoma nyavu, tunafanya vile lakini inaonekana inakosekana ile sustainability, uendelevu unakosekana.

Mheshimiwa Spika, sayansi ya uvuvi inataka tulinde maeneo ya mazalia na makulia ya samaki na ndiyo maana Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, Ibara ya 43(f) ikatuelekeza Serikali wazi wazi, kwamba tuhakikishe tunalinda maeneo ya mazalia na makulia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la mamlaka Mwenyezi Mungu akitujalia insha Allah litakwenda kuwa ni mwarobaini mzuri sana. Kwa hivyo kusudio hili tumeanza kuchukua maoni ya Waheshimiwa Wabunge na tutaendelea sisi, tutapitisha katika vikao vyetu vyote vya kiwadau, tutaona linalowezekana kufanyika. Hili unajua automatically linakwenda kuondoa hizo hofu zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukishakuwa umelinda maeneo ya mazalia na makulia una uzalishaji mzuri, kuanzia baharini kule katika matumbawe kuja huku katika Maziwa na mpaka Nyumba ya Mungu, Hale mpaka Jipe, yote hayo yanaingia mle, hapa mambo mbona yatakuwa mazuri sana na uzalishaji utakuwa ni mzuri sana. Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge wenzangu wasiwe na wasiwasi wavuvi wenzangu juu ya jambo hili, kwani tumelichukua na tutalipa uzito na tutaona kusudio hili linawezaje kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninayo mengi ya kusema, lakini haya ndiyo yaliyokuwa mazito. Mengine nitayajibu kwa maandishi. Nataka nimalizie nisichukue dakika zako nyingi. Kwa kuwa nimezungumza juu ya mundombinu ya mifugo na nia yetu kama Serikali, najua wako watu wangependa kuzungumzia minada, wengine wangependa kuzungumzia magomvi kati ya wakulima na wafugaji yaliyosababishwa na mambo ya maji ukosefu wa mabwawa, nafahamu. Najua pia wako watu wangependa kuzungumzia malisho, nimeyasema hapa naomba watuunge mkono ili tukapunguze kero hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua sayansi ya kuondoa hii migogoro ya wakulima na wafugaji, naiona ni nyepesi tushikamane, tutaiondoa, watu waishi kwa amani. Leo najua njia za mifugo huko Wilayani kote njia za mifugo zinajulikana. Kama zinajulikana kupita mle katika zile njia za mifugo kama tunafanikiwa kwenda kutengeneza chombo ambacho kitakuwa kikisimamia ile miundombinu ya mifugo na wafugaji ambao wako tayari tukaenda tukashirikiana nao vizuri, wakawa wanachangia vizuri, sasa ugomvi utatokea wapi? Kama mtu anatafuta maji? Maji si ndiyo haya hapa, kama mtu anatafuta malisho, malisho si ndiyo haya hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafahamu kwamba hata kaka yangu Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa Mstaafu wa zamani Mheshimiwa Innocent Kalogeris angetamani aishike tena leo shilingi kama alivyofanya mwaka jana, lakini asiwe na wasiwasi, mawazo hayo na fikra hizi zilizotolewa hapa zinatosheleza kabisa kujenga msimamo wa kwamba tunakwenda pazuri.

Mheshimiwa Spika, najua hata rafiki yangu Mgosi Wandima, Mheshimiwa Reuben, angetamani ashike shilingi kwa ajili ya mnada wake pale Handeni Mjini. Kaka suluhisho ni hili hapa, tushikamane hakuna hoja tena. Ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mwisho, naomba nimalizie kwa maneno yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumza hapa mtani wangu Mheshimiwa Luhaga Mpina juu ya hoja mbili; unajua nilikuwa sitaki kusema, lakini sasa ametaja majina ya wakubwa, nataka nimfafanulie baadhi ya mambo. Hoja ya kwanza kwa sababu amemtaja mpaka Rais ya Awamu ya Tano ile ya kuchoma moto vifaranga. Unajua hizi sheria zinatekelezwa halafu katika utekelezaji wa sheria yako mambo ya busara na hekima, namna ya kufanya vile vitu. Sheria inasema tu–destroy kwamba mtu kama amekosea akaingiza vifaranga unatakiwa ku–destroy, namna ya ile destruction, sheria haikusema uchome moto, uwachimbie katika shimo, uwafanyaje sheria haikusema hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ugomvi wa pale ulikuwa ni nini? Ni kwa nini vifaranga vichomwe mbele ya macho ya watu? Namshukuru amezungumzia juu ya animal welfare (haki ya wanyama), angalia mgongano wa mambo hapo, aliyekosea ni nani? Aliyekosea ni mwingizaji wa vifaranga au vilivyokosea ni vile vifaranga? Sasa kwa nini uvichome moto mbele za watu? Simple, kwa hivyo hapa issue inawezekana vinachomwa moto kila siku huko, yawezekana kabisa, lakini kwa nini unavichoma moto mbele za watu? Hii ndiyo hoja.

Mheshimiwa Spika, binadamu wameumbwa siyo mnyama, siyo hayawani, binadamu siyo hayawani, viumbe vile vina haki yake na namshukuru amezungumza vizuri wakati alipokuwa akitetea ng’ombe ambao ni kweli Kanuni ile tumeisaini ya kuilinda haki za Wanyama. Sasa haki za wanyama ni pamoja na kutokuwachoma hadharani. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pilli la samaki. Anataka mimi niseme, unajua Mpina mimi nakuheshimu sasa siwezi kusema kila kitu wewe ulikuwa bosi wangu pale Wizarani. Sasa mimi niseme ukweli, mimi ni muungwana, msema ukweli ni mpenzi wa Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo na yeye anajua tumekaa vizuri sana, mimi na yeye pale wakati niko katika winding up pale Wizarani kwa namna ambavyo namheshimu, kwanza jana nilimpigia simu Mheshimiwa Mashimba Ndaki, kumuuliza bwana, kesho tunakwenda katika hoja, nimeliona jina lako, vipi Mzee unataka kuchangia? Akaniambia Mheshimiwa Waziri, sina haja ya kuchangia bwana. Akaniambia kwamba yeye atachangia kwenye kilimo, nikamwambia bwana mimi nakutakia kila la kheri kwa sababu nilitaka nijue anataka kuchangia kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa leo nikiwa na watendaji pale Wizarani, Mheshimiwa Luhaga Mpina, nilimpigia simu niseme ukweli na msema ukweli mpenzi wa Mungu na namfurahia amewataja watendaji wengi wa Wizara ambao na mimi nilikuwa nao pale Wizarani. Sasa hivi kama saa moja tu iliyopita, nikamuuliza bwana mzee nimeona jina lako unataka kuchangia, una jambo lolote nikusaidie? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, akaniambia, hapana bwana. Mimi ni kweli naenda kuchangia, nikamuuliza kuna kheri shehe? Akaniambia ipo kheri kubwa sana wala usiwe na wasiwasi. Sasa simkatalii yeye kuchangia hapa Bungeni kwa kuwa ni haki yake, lakini nataka nimkumbushe ananiambia kwa nini sisemi juu ya rula ilivyotumika pale kantini? Sasa Mheshimiwa Mpina wakati mwingine tunakaa kimya, maana kukaa kimya nako ni busara. Samaki yule akishapikwa anapoteza shepu, anapoteza size, sayansi ya samaki haielekei huko. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, samaki yule aliyempima hapa Bosi wangu wa zamani Mheshimiwa Mpina, alikaangwa, kapita katika nyuzi joto nyingi sana. Kwa hivyo ameshapoteza ile hali yake, yaani ile physical appearance yake imepotea kabisa, huwezi kupata uhalisia. Sasa alitaka mimi wakati ule nikiwa Naibu nimwambie Mzee unakosea hapo. Katika hali ya kawaida na nadhani kwa kuwa sikumwambia hivyo wakati ule sikupishana naye, sikugombana naye, ndiyo maana mimi Abdallah Ulega hadi hii leo nipo katika podium hapa kama Waziri. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, mantiki yake ni nini? Mantiki yake ni kwamba, kama ningeligombana nae wakati ule ningeliambiwa mimi ni mkosefu, sina adabu, ni mjeuri, unagombana na bosi wako, labda saa hizi nisingekuwa mahali hapa. Itoshe kusema kwamba Waheshimiwa Wabunge kwa heshima kubwa na taadhima nawashukuruni sana, ameondoka mke wangu Mama Tulia hapa na furaha kubwa sana kwa sababu amesikia michango mizuri ya pongezi, matumaini, shukurani na kunitakia kheri katika kutekeleza jukumu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwaahidi kwamba kazi imeanza. Mtafurahi yaani show show vijana wa mjini wanasema, naombeni uungaji mkono wenu hata wale kama nilivyokwishasema waliokuwa wanafikiria kushika shilingi vinginevyo iwe nje ya hoja hizi, lakini naomba waniamini, ninaye Naibu Waziri mzuri sana, comrade Silinde. Mheshimiwa Silinde alikuwa akiniheshimu sana toka tukiwa wote Manaibu Waziri hapa sana. Leo hata mimi najua nilipoteuliwa na yeye kuwa Naibu wangu nilijiuliza hee! Hii nchi kweli inaona. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, niruhusu nimalizie hizi dakika zangu mbili niwaambie Waheshimiwa Wabunge kidogo; katika Naibu Mawaziri sisi wakati ule nikiwa Naibu Waziri, tuna utamaduni wetu, kila mahali mnapokuwa wawili, watatu anapatikana kiongozi. Sasa tukakaa Manaibu Waziri tukaulizana nani anakuwa Mwenyekiti wetu? Mheshimiwa Silinde akanyoosha mkono wa kwanza, wote tukiwa Manaibu, akasema ahaa jamani hilo nalo la kuulizana, Mwenyekiti hapa si Abdallah Ulega bwana Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Hiyo nawaonyesha namna ambavyo toka huko nyuma tumekuwa tukishirikiana na kuheshimiana sana. Kwa hivyo, nawapa matumaini, ninaye Profesa Riziki Shemdoe, wote wanamfahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huyu jamaa Profesa Riziki Shemdoe, ni Mgosi Wandima, kule kwa Lushoto kuna kitu kinaitwa Muku, wanajua Wasambaa hapa. Muku wanakula watu wa kazi, akila hiyo hachoki kufanya kazi, ndiyo huyu jamaa. Kwa hiyo saa nane ya usiku nikimpigia simu anaitika simu yangu, nikimwandikia meseji yuko hewani. Nataka niwahakikishie, sasa kuna maneno hapa naogopa kuyasema, nikiyasema itakuwa hatari, lakini kwa mchanganyiko huu jinsi ulivyo mzuri ni kama ile timu iliyoingia nusu fainali juzi hapa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, basi, kwa kuwa naomba nisishikiwe shilingi, niseme tu kwamba ni kama zile timu mbili ambazo zimefanya vizuri sana hapa juzi. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Pili, naipongeze sana Serikali kwa jitihada zake za uchumi wa viwanda kwenye nchi yetu. Pia, nampongeza Mheshimiwa Waziri na kwa namna ya pekee kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye hoja moja kwa moja. Naomba Mheshimiwa Waziri anieleze ni namna gani iliyo rahisi kabisa viwanda vinaweza kupata malighafi ya gesi kwa ajili ya uzalishaji wa umeme? Mfano, Kiwanda tarajiwa cha marumaru (tiles) cha Goodwill Ceramic Tiles kinahitaji gesi na wawekezaji hawa wapo tayari kabisa kujenga bomba kwa gharama yao wao wenyewe (Mkopo kwa TPDC): Je, Wizara itasaidiaje kuharakisha jambo la namna hii?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wawekezaji hawa pia wa Goodwill Ceramic pia wameomba bei ya gesi iweze kuwa stable (imara). Naiomba Wizara ya Viwanda isaidie pia katika kuhakikisha inashirikiana na Wizara ya Nishati na Madini kuharakisha jambo hili pia. Mwisho, naipongeza tena Serikali kwa jitihada hizi na kusisitiza kuwa jitihada hizi ziendelee kwa manufaa ya Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yoyote na mimi nianze kwa kuipongeza Serikali na kuunga mkono hoja hii. Lakini kutokana na ufinyu wa muda naomba nizungumze mambo makubwa matatu halafu nitajielekeza katika ya mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo yenyewe ni kama ifuatavyo, na ningeomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji wayachukue mambo haya
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kariakoo ni sehemu yetu ya biashara tunayoweza kuiita ni sehemu ya biashara ya kimataifa. Hivi sasa Kariakoo inahudumia zaidi ya nchi tano za Kiafika ikiwa na sisi wenyewe wa ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu tulikuwa na tatizo bandarini, lakini hapa karibuni kwa takribani wiki mbili, tatu, mwezi tatizo la upatikanaji wa mizigo kwa ajili ya soko letu hili la Kariakoo, kwa maana eneo la Kariakoo limejitokeza kutokana na agizo lile la kwako Mheshimiwa Waziri la TBS. Nomba nikueleze kuwa jambo hili siyo baya, lakini nataka hili jambo la TBS uweze kuliweka vizuri na elimu kwa wafanyabiashara wale iende sawasawa.
Mheshimiwa Waziri, wafanyabiashara wa Kariakoo wengine ni wafanyabiashara wadogo wadogo ambao ni wanakusanya mitaji yao wanaunganisha katika kontena moja. Mmoja tu anapokosa kukutana na SGS, wakala wetu shida kubwa inatokea pale bandarini. Nataka nikuambia storage ya wafanyabiashara wale wa Kariakoo hivi sasa imekuwa kubwa sana na mitaji yao inakatika.
Nakuomba sana jambo hili uliingilie uone ni namna gani ya kuweza kuwasaidia ili waweze kuendesha maisha yao na hatimaye biashara iendelee kuweza ku-propel katika eneo hili la biashara la Kariakoo.
Mheshimiwa mwenyekiti, naomba nizungumzie BRT, nimeiona katika Mpango wa Maendeleo wa Mwaka huu wa 2017/2018. Naomba nisisitize ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja Mkuranga, alisema kwamba BRT itakwenda mpaka Mkuranga, itavuka pale maeneo ya Mbagala. Naomba iende kwa sababu tunalo eneo zuri la Serikali, linaweza kutusaidia kwa kazi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana yuko msemaji mmoja hapa alisema hakuna viwanda vipya. Nikuombe Mheshimiwa Waziri uwachukue baadhi ya Wabunge walete kule Mkuranga wakione kiwanda cha Good Will Ceramics kipya ambacho zaidi ya shilingi bilioni 200 zimewekwa pale na tunategemea zaidi ya wafanyakazi 4,500; watu wa Mtwara, Lindi wanajua kiwanda kile cha kilometa moja kinachojengwa pale Mkuranga, naomba jitihada hizo zifanyike zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba pia ulitangaze eneo la Mkiu kuwa ni eneo rasmi la viwanda. Tunazo ekari nyingi pale hazihitaji compensation, walete. Na naomba uwabadilishe mindset Waheshimiwa Wabunge hawa, mambo ya kuwaza kiwanda kikubwa sana kama kile cha Mkiu Mkuranga waachane nayo. Viwanda vidogo vidogo vya dola 5,000, 10,000, ardhi tunayo pale, waje wawekeze katika kubangua korosho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie na maneno yafuatayo ya ahadi ya Mheshimiwa Rais. Wakati Mheshimiwa Rais anachukua nchi hii mwezi Novemba, 2015 aliahidi kupambana na rushwa, aliahidi kufanya kazi kubwa ya kuzuia matumizi yasiyokuwa mazuri ya pesa za umma pamoja na kushughulika na watu wasiokwepa kodi. Mheshimiwa Rais alipokuja Mkuranga alieleza wazi hana tatizo na wafanyabiashara akitumia uwanja ule wa Bakhresa. Watu leo humu ndani wanazungumza kwamba Serikali hii haina urafiki na wafanyabiashara.
Mheshimiwa Rais aliwaeleza wazi mfanyabiashara anayelipa kodi huyo atakuwa ni rafiki yake, lakini mfanyabiashara asiyelipa kodi hana urafiki naye. Nataka niwaambieni IMF wametoa ripoti Jumatatu, timu ile inaongozwa na mtaalam mmoja anayeitwa Mauricio Villafuerte. Huyu bwana ameeleza wazi, ameeleza namna nzuri ambayo tunakwenda nayo, lakini wametushauri pia juu ya kujaribu kurahisisha kidogo juu ya mzunguko wetu wa fedha na mengineyo, lakini wametupongeza na wamefikia hatua nzuri ya kuwaambia Watanzania kwamba hata madeni ya nje na mengineyo sasa tuko vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka nimalizie na maneno ya Mwenyezi Mungu katika kitabu kitakatifu cha Qurani. Mwenyezi Mungu subhana wa ta’ala anasema katika Qurani tukufu kama ifuatavyo; “Na wale wanaojitahidi kwa ajili yetu tutawaongoza njia zetu. Nasema fanyeni kazi basi ataona Mwenyezi Mungu vitendo vyenu na Mtume wake na waumini wataviona vitendo vyenu. Enyi wanangu wala msikate tamaa na rehema za Mwenyezi Mungu, hawakati tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu isipokuwa watu waliokosa imani.”
Mheshimiwa Mwenyekiti wale watu waliokosa imani wote wamepotea. Leo mkubwa mmoja amekuja humu ndani anahangaika, anaweweseka, nazungumzia shilingi milioni 10, kama anazitaka zile shilingi milioni 10 aje timu kubwa huku CCM asikate tamaa wamebanwa.
heshimiwa Mwenyekiti, nashukura sana naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nikushukuru kwa nafasi hii niliyoipata ya kuchangia bajeti ya Wizara yetu hii ya Maliasili na Utalii. Pia naomba niendelee kumpongeza Waziri, Mheshimiwa Profesa Maghembe na kaka yangu Naibu Waziri, Mheshimiwa Mhandisi Ramo Makani. Nataka tu niwaambie kwamba wafanye kazi na wala wasitishike na haya manenomaneno mengine ya kuwavunja moyo na sisi tunaelewa juu ya weledi na uwezo wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine hata mimi naanza kushawishika kuunga mkono wale wanaofikiria kwamba kabla hatujaingia kwenye jengo hili tuwe tunapimwa pale kama tumevuta hata marijuana hivi. Katika hali ya kawaida, kijana hata kama umepigiwa kura na kuaminiwa na wananchi ukaenda kumtukana mzee wa namna ile na kumuita majina ya hovyo, lazima utakuwa una tatizo kidogo katika akili yako, siyo wa kawaida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii imedhihiri hata jana, yupo mwenzetu mmoja hapa wa kutoka katika chama ninachotoka mimi amezungumza mambo ya ajabu sana hapa. Unaweza ukaona ni kwa namna gani watu hawaelewi ni nani katika nyumba hii ameingia bila ya chama kilichomleta hapa. Wote kwa umoja wetu, iwe wa upinzani, iwe wa chama kinachotawala, sisi tumezaliwa na vyama vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima sisi kama viongozi tujue wajibu wetu na hii michezo haitaki hasira. Wala usidhani kwamba wewe ukiwa na hasira sana ndiyo hoja yako itafanikiwa, la hasha! Wakati mwingine unajielekeza tu katika kukata udugu. Nataka nikuhakikishie sisi kule kwetu tunasema mkataa udugu kala hasara huyo! (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme juu ya misitu na Mheshimiwa mama Mariam Kisangi amesema vizuri hapa juu ya msitu, mkaa na vitu vya namna hiyo. Nafahamu kwamba mkaa, kwanza naomba ni-declare interest, mimi ni mwana mazingira na profession yangu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni Shahada ya Sayansi ya Mazingira. Nina weledi mzuri na mkubwa sana juu ya masuala ya mazingira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Dar es Salaam nyumbani kwetu na Mkuranga yake watu wanaendelea kutumia nishati ya mkaa na Serikali tunajua kwamba inapiga vita matumizi ya mkaa. Nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba nguvu tunayoitumia katika kupiga vita matumizi ya nishati hii ya mkaa, tutumie nguvu hiyohiyo katika kuhakikisha tunawatafutia nishati mbadala wananchi hawa. Watu wanapata shida sana, watu hawaelewi wafanyaje, tunawaambia watumie gesi, hata elimu yenyewe ya matumizi ya gesi inafahamika? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya gesi hayakuanza leo, watu walio wengi, hata wasomi wenyewe wanaogopa kutumia majiko ya gesi maana yameua watu wengi sana katika nchi hii. Wewe mwenyewe unafahamu mwaka mmoja, mwishoni mwa miaka ya tisini, hoteli ya Kibodi ya Dar es Salaam katikati ya mji iliungua moto kwa sababu ya jiko la gesi. Sasa tufanye jitihada ya kutoa elimu, kabla ya kusema kwamba watu hawa wasitumie mkaa, tumefanya jitihada gani ya kuwaelimisha, tumefanya jitihada gani ya kupeleka nishati mbadala? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti imezungumzwa hapa kodi ya vitanda nami naunga mkono hoja ya kodi hii ya vitanda ni lazima itazamwe, lasivyo yanaendelea kuwa ni yale yale ya kutokuwasidia watu hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa Msitu wa Mwandege pale Mkuranga, kile kimekuwa ni kichaka cha majangili. Mkuranga yenyewe imetajwa kama ni eneo ambalo si salama sana. Wewe mwenyewe unafahamu kwamba walikamatwa pale watu zaidi ya 50 na bunduki, wamezificha. Haukupita muda mrefu Benki yetu ya NMB pale Mkuranga ikavamiwa na majambazi. Hatujakaa muda mrefu Benki ya Access pale Mbagala Rangitatu ikavamiwa na majambazi. Hawa wote wanakimbilia kwenye msitu huo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kumwambia Mheshimiwa Waziri, kama tunashindwa kwa kuwa hatuna pesa za kutosha za kuutunza msitu ule Dar es Salaam imejaa, ni kweli. Eneo lile ni kubwa sana linachukua vijiji zaidi ya vinne Mwandege yenyewe, vikindu, Mlamleni Luzando na kwingineko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitenge eneo lile dogo tupate eneo la kutosha pale tujenge kituo cha kisasa, watu wanaotoka Mikoa ya Kusini hawana haja ya kwenda na mabasi yao mpaka Ubungo mpaka Dar es Salaam. Waishie pale Mkuranga waingie kwenye shuttles waende Dar es Salaam hii itatusaidia tutapata pesa tutafanya msitu ule kuwa ni botanical garden. Badala ya kuuweka tu vile kuwa ni kichaka cha majangiri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niseme juu ya ng‟ombe na hasa hao wanaoingia katika maeneo ya hifadhi. Juu ya wakulima na juu ya ng‟ombe imeshazungumzwa sana. Naomba niseme wazi hapo kwetu sisi ng‟ombe ni kitu kipya, hapa nasema jambo jipya kabisa. Kwanza zamani tulikuwa tunamwita mdudu, leo tumeletewa ng‟ombe wengi sana na ugomvi ni mwingi sana pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama inavyosemwa na wenzangu ni lazima tutafute suluhisho la kudumu la jambo hili, wakulima wetu hawamjui ng‟ombe na wala hawana haja ya kumjua. Eee!
Mheshimiwa Mwenyekiti, issue ya misitu tena katika mazingira naomba nimwambie jambo moja Mheshimiwa Waziri kwamba hili jambo liwe ni two way traffic. Mpaka hivi sasa sisi tunatumia nguvu nyingi sana juu ya kulinda hifadhi zetu lakini bado hatujajifunza. Nilipokuwa Mkuu wa Wilaya kule Kilwa ninao mfano mzuri sana wa Kijiji cha Nanjilinji, tulikuwa na jambo kule la hifadhi ya misitu ya jamii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Nanjilinji kimefanikiwa sana katika uhifadhi wa jamii wa misitu yake. Leo mtu akikuona umeshika fito hawezi kukuelewa, lazima atakuchukulia hatua yeye mwenyewe pasipo kwenda na askari wa games wala jambo la namna gani. Kwa hivyo, hebu tuiangalie sera yetu vizuri hapa, namna ambavyo tunaweza tukawashirikisha jamii tukawasaidia ili wao wenyewe wawe walinzi wa rasilimali hizi badala ya kutumia maguvu mengi sana ambayo wakati mwingine wala hayana tija na yanatupotezea pesa zetu nyingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji nawahakikishia watani zangu Wasukuma na wengineo watoe mifugo ile; kule South Africa, Limpopo kwenye hifadhi ile maarufu kabisa ya Great Kruger pametokea tatizo. Ng‟ombe wote wamepata matatizo ya magonjwa ya miguu na midomo na ule ugonjwa sasa umeshaanza kutokea kwa wanadamu na umeshaingia mpaka Zimbabwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipofanya jitiada hao ng‟ombe watakufa na watu nao watakufa na mazingira yetu yataharibika. Kwa hivyo, ni lazima watu kukubaliana na jambo hili, ni kinyume cha utaratibu kabisa kufanya jambo la namna hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalize na utalii. Nafasi ya Tanzania katika utalii ni nzuri, tunahitaji kufanya jitihada zaidi ili kuhakikisha kwamba utalii wetu uweze kuwa na faida hasa ya kuondoa umaskini. Juzi hapa China tarehe 21 umemalizika Mkutano wa World Tourism Organization, ulifanyikia Beijing pale, moja ya jambo kubwa kabisa lililokubaliwa katika mkutano ule ni kuhakikisha kwamba utalii uondoe…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye mjadala huu unaoendelea wa hali ya uchumi lakini pia na bajeti yetu kuu ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu subhanahu wataala, kwa kunijalia siku hii ya leo kuwa ni siku ya kipekee kwangu mimi Abdallah Hamisi Ulega na familia yangu ikiwa ni pamoja na mke wangu kipenzi Bi. Mariam Abdallah kwa kutujalia kupata mtoto, tena mtoto wa kike. Kwa kweli, nazidi kuthibitisha kwamba akinamama ni wastahamilivu, wavumilivu, ni watu wenye uwezo mkubwa sana kila mahali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mke wangu huyu mwaka wa jana alipoteza mtoto wa umri wa miezi tisa. Mwaka juzi pia alipoteza mtoto wa umri wa miezi tisa. Hakukata tamaa, hatimaye mwaka huu wakati wake umefika na mambo yamependeza. Huyu mtoto katika moja ya jina zuri nitakalompa nitampa jina la Tulia. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni katika ile kuthibitisha kwamba ninyi akinamama mnaweza. Wallah nataka nikuhakikishie kwa mikasa hii aliyoipitia mke wangu kipenzi, ningekuwa mimi ningekata tamaa, lakini yeye hakukata tamaa kama vile ambavyo wewe hukati tamaa na hawa manyang‟au wanaotaka kutusumbuasumbua humu ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, naendelea kumpa pongezi sana mke wangu kipenzi kwa kazi kubwa sana anayoifanya kwa ajili yangu na kwa ajili ya nchi hii ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze katika kuchangia bajeti. Kwanza kabisa hali ya uchumi na nashukuru sana baadhi ya wasemaji wamesema juu ya hali ya uchumi na mimi nitasema kwa muhtasari sana. Ombi langu kubwa kwa Mheshimiwa Waziri wetu wa Fedha atakapokuja kufanya winding up hapa atueleze, maana sitaki kusema kwamba sisi watu wa Mkoa wa Pwani tumewekwa katika bahati mbaya ya kuwa matajiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuwa tajiri ni jambo jema sana lakini nataka atuambie ni criteria gani alizotumia za kutufanya sisi kuwa ni miongoni mwa mikoa matajiri. Maana nilikuwa napitia kwamba ni vigezo gani vinaweza vikamfanya mtu akaambiwa wao ni matajiri, per capita income au huduma za kijamii? Sisi kule kwetu huduma za kijamii hali ni mbaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, mmoja katika wasemaji waliowahi kusema siku ya jana nilipokuwa nikifanya mijadala yangu, anasema kwa kuwa ninyi mpo karibu na Dar es Salaam, hospitali za rufaa ziko karibu, nikamwambia hospitali ya rufaa si ya watu wa Mkoa wa Pwani, Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili ni ya watu wa Taifa zima la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni nini hasa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwingine akaniambia ninyi mna lami inapita kila mahali katika mkoa wenu. Nikamwambia si kweli, sisi kutoka Nyamwage - Utete tuna shida kubwa, kutoka Mkuranga Mjini - Kisiju tuna shida kubwa, kutoka Bungu - Nyamisati kuna shida kubwa, kutoka Mlandizi - Makofia Bagamoyo kuna shida kubwa, kutoka Mlandizi - Mwaneromango - Mzenga – Vikumbulu - Mloka pana shida kubwa, sasa kwa nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, hatuna haja ya kuwa na wasiwasi isipokuwa tunataka tujue ugunduzi gani uliofanyika katika Mkoa wa Pwani ukawafanya watu wa Mkoa wa Pwani leo wakawa na maisha makubwa ya kuwashinda wengine katika Taifa letu? Maana sisi tuna korosho na korosho yenyewe watu wa Mtwara wanatuzidi kwa mbali, watu wa Lindi wanatuzidi kwa mbali, ni nini hasa, ni vigezo gani, atuambie waziwazi ili na sisi tuongeze jitihada zetu. Pale ambapo atapataja kwamba ninyi watu wa Mkoa wa Pwani mahali hapa mko vizuri, basi inshallah sisi tuongeze nguvu zetu na tufanye vizuri zaidi ili tuweze kuwa na maisha bora ambayo Taifa letu linataka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hilo, naomba sasa niende kwenye maji. Kama walivyosema wenzangu, naomba sana Mfuko wetu wa Maji uendelee kuongezewa nguvu. Tazama mimi katika Jimbo langu la Mkuranga uko mradi wa muda mrefu wa pale Mpera na Kimbiji, unahitaji shilingi bilioni 12 tu. Tutazipataje pesa hizi bila ya kuongeza nguvu katika Mfuko wetu wa Maji?
Mheshimiwa Naibu Spika, nina shida kubwa ya maji katika Mji wa Mkuranga, hatuwezi kupata pesa ya kuweza kuusababisha mradi ule wa Mkuranga unaohitaji takriban shilingi bilioni 2.2 uanze. Tunasema tunaendelea kufanya mazungumzo na kampuni ya Strabag ya Australia kwamba hii ndiyo itakayotusaidia, wasipokubali hawa kutusaidia maana yake watu wa Mkuranga Mjini waendelee kuwa na shida ya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana kwa heshima kubwa na taadhima, nguvu zetu tuzielekeze katika kuongeza Mfuko wa Maji ili tutatue kabisa tatizo la maji ambalo linawakabili hasa hawa niliowasifu pale nilipokuwa naanza kutoa hotuba yangu, akinamama. Unaposaidia tatizo la maji unawasaidia akinamama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ningeomba sana tuongeze nguvu zetu katika utalii. Naomba niseme kwamba suala la utalii kuongezewa kodi zote hizi ni tatizo kubwa. Katika takwimu inaonesha kwamba bajeti yetu ya 2015/2016 sekta ya utalii iliongoza kwa asilimia 25. Katika mwaka wa 2014/2015, inaonesha kwamba pesa za kigeni takriban shilingi trilioni 8.3 zimetoka katika utalii. Inaonekana kwamba mwaka 2015 takriban ajira milioni moja, laki mbili na tisini na nne elfu zimetokana na utalii. Leo hii utalii huu umeongezewa kodi nyingi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika nchi zetu za Afrika Mashariki Wakenya wameondoa kodi mbalimbali katika utalii na nia yao ni kuongeza utalii katika nchi yao, nia yao ni kuongeza idadi ya watalii, ajira na kipato chao. Tusipofanya jitihada ya kuondoa kodi hizi utalii utashuka. Tazama katika utalii kazi ambazo zimepangwa kufanywa na Watanzania peke yake ni pamoja na kukodisha magari, wakala wa safari (travel agents), kupanda milima na waongozaji watalii na zote zimewekewa kodi. Kwa hiyo, hii itasababisha kupunguza idadi ya watalii, projection yetu ya kupata idadi kubwa ya watalii itapungua.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapiga kelele hapa ya kupata pesa za kutosha kwa ajili ya miradi yetu ya maji, afya, ambapo afya imeachwa mbali katika bajeti hii. Tutazipataje hizo pesa kama tunaongeza kodi ambazo zitawakimbiza watalii wetu? Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa positive measure aliyoifanya ya kuongeza kodi ya utalii katika vyombo vya usafiri wa anga lakini apunguze kule kwingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, narudia tena kumpongeza sana mke wangu na kuwapongeza akinamama wote. Naunga mkono hoja hii na ahsanteni sana.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru sana kwa kupata nafasi ya kuchangia katika mjadala huu unaohusu Kamati yetu ya Viwanda na Biashara na Mazingira lakini nikienda sambamba na ile ya Mitaji na Uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nichukue fursa hii kupongeza sana Kamati yetu, imefanya kazi nzuri yenye kupendeza ambayo imeeleza mambo mbalimbali hasa hii ya Viwanda na Biashara ambayo ningependa nijielekeze kwake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi naomba niwe shuhuda mzuri sana wa Tanzania ya viwanda. Katika Jimbo langu la Mkuranga mpaka sasa nina viwanda 56 vyenye kufanya kazi na nina viwanda 11 ambavyo wakati wowote vitakamilika. Katika hivyo 11, kimoja ni kile kipya na kikubwa kushinda vyote katika Afrika Mashariki na Kati, kiwanda cha tiles ambapo tutakuwa na uhakika sasa wa kutokuagiza tiles kutoka nje ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakuwa na uwezo sisi wenyewe katika nchi yetu kupata huduma hii bila kuagiza kutoka mahali kokote. Kwa fursa hii kwa kweli kabisa napenda niipongeze sana Serikali yetu kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya ya kuwavutia wawekezaji wale na wakaja katika Jimbo letu la Mkuranga na kuwekeza pesa zao nyingi kabisa juu ya kujenga kiwanda hiki kikubwa cha tiles.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema ukweli uwepo wa viwanda umetuinulia sana uchumi wetu sisi watu wa Mkuranga na nchi kwa ujumla wake. Mwaka jana 2016/2017 mwaka huu ambao tunamalizana nao tuliweka kadirio la kupata service levy isiyopungua milioni 500 na sasa tutakuwa na uhakika wa kupata service levy isiyopungua bilioni moja katika huu mwaka wa 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima niseme ukweli na hapa ndipo nilipokuwa nataka nisisitize sana, kwamba bado tunayo fursa kubwa zaidi ya kuwa na viwanda vingi zaidi, hasa hususani katika Jimbo la Mkuranga na sehemu zingine katika nchi. Kazi kubwa ambayo ningependa niiseme hapa ni kwa wenzetu wa Wizara ya Nishati na Madini, wajitahidi sana katika kuhakikisha nishati hii ya gesi, ya umeme, iweze kuwa ya uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nimekikosa kiwanda pale Mkuranga cha kutengeneza nguo katika eneo la Dundani. Mwekezaji amekuwa yuko tayari kabisa ataajiri vijana wasiopungua 14,000 lakini sharti la kwanza anataka umeme wa uhakika. Sasa pamoja na jitihada kubwa sana za kuwavuta wawekezaji zinazofanyika na wao wanaitikia, lakini bado tunayo changamoto kubwa ya nishati. Kwa hivyo wenzetu wa nishati wajitahidi wahakikishe mipango yao ya kusambaza gesi katika viwanda vyetu iende sambamba na mahitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mathalani katika viwanda hivi vyote 56 hakuna kiwanda hata kimoja leo kinachotumia gesi na hilo bomba la gesi limepita hapo hapo Mkuranga. Kwa hivyo wenzetu ni lazima watuambie; nimemsikia Naibu Waziri asubuhi anasema kuna zaidi ya bilioni tano ambazo zitaelekezwa katika kwenda kusambaza gesi majumbani katika maeneo ya Tabata na Sinza na kwingine kule Dar es Salaam, lakini hakueleza ni kiasi gani cha fedha ambacho kitatumika kwenda kutengeneza mtandao wa mabomba ya kusambaza gesi katika viwanda hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kupata huduma hii ya nishati kwa bei nzuri na hatimaye uzalishaji wa bidhaa katika viwanda vile uwe ni wa gharama nafuu na hatimaye kumsaidia Mtanzania mlaji wa zile bidhaa zinazozalishwa katika viwanda vile ili aweze kupata zile bidhaa kwa bei nzuri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wetu alipokuja katika kiwanda cha Bakhresa aliagiza jambo hili, aliagiza kwa sababu watu Bakhresa food industry wameomba wapate gesi kwa muda mrefu na bado hawajafanikiwa mpaka hivi sasa. Jambo ambalo linapelekea uzalishaji wa bidhaa katika viwanda mbalimbali katika maeneo yetu unakuwa ni wa gharama kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo tuwaombe wenzetu watuambie ni namna gani, viwanda viko vingi sana, vinaingia kila siku ya Mwenyezi Mungu lakini je, tumetengeneza mazingira ya namna gani ya kuweza kuvisaidia kupata huduma hii ya gesi na nishati kwa urahisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwezekana nawashauri na kuwaomba wenzetu hawa wa nishati na madini waone umuhimu wa kuiweka Mkuranga kuwa hata na substation yake ya umeme, uwezekano huo upo na wala hakuna tatizo lolote la eneo wala hakuna tatizo lolote la upatikanaji wa gesi. Gesi tap ziko pale valve namba 12 na 13 katika maeneo ya Mbezi na Mkiu zinapatikana kwa wingi kwa hivyo tunawaombeni sana mtuweke substation pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati huu wa viwanda ni lazima kama ilivyopendekezwa na Kamati katika ukurasa wake wa 50 juu ya elimu ya ufundi. Vijana wetu wengi sana wanakwenda kuwa vibarua katika viwanda hivi, lakini tunaomba sasa ikiwezekana na wenzetu wa elimu muone umuhimu wa maeneo kama haya ya viwanda kuyapa uwezekano wa kuwa na vyuo vya elimu, ili vijana wetu waweze kupata elimu na hatimaye waweze kwenda kuwa na uwezo wa kwenda kuajiriwa katika viwanda vile. Hivi sasa unaweza ukakuta ni asilimia ndogo sana ya vijana wa Mkuranga ambao wanafanya kazi katika viwanda hivyo. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri anayehusika pia alitazame hili jambo kama ilivyopendekezwa na Kamati yetu ya Viwanda na Biashara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia ningeomba sana masuala haya ya ukuaji wa viwanda na sisi tumejiandaa vizuri na tayari maeneo yapo ya kutosha. Mathalani tunalo eneo pale katika Kijiji cha Dundani, zaidi ya ekari 700 na Waziri wetu wa Viwanda na Biashara amekuwa akilitaja kila mara. Sasa afanye kazi ya kuhakikisha wananchi wale zaidi ya miaka minne sasa, asiwe anakuja tu kaka yangu Mwijage kulitangaza lile eneo, awalipe fedha za fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wale watu wamezuiwa kufanya chochote katika eneo lao, sasa ni miaka minne hawawezi kuendeleza chochote, hawazalishi chochote, hawasafishi maeneo yao ni kwa sababu wamejitolea eneo lao lile liwe ni eneo la viwanda. Sasa wale wananchi wamekata tamaa, ni lazima tuone ni namna gani either hawa wa Mkuranga au ni kwingineko kokote katika nchi watu walikojitolea katika kuhakikisha kwamba Tanzania ya viwanda inapatikana, basi mambo haya yakamilike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana nisisitize tena kwa mara nyingine juu ya kupatikana kwa nishati ya gesi katika viwanda vyetu ili uzalishaji uwe wa gharama nafuu. Ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naanza kwa msemo wa Waswahili tunaosema kwamba “Haja ya mja hunena muungwana ni vitendo.” Namshukuru sana na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya na kila mmoja anaona kabisa. Tuseme ukweli kwamba ni lazima tukubaliane kwamba hatuwezi kufanikiwa bila ya kufunga mkanda na ku-sacrifice kwa ajili ya kizazi cha leo na cha kesho. Wazungu wanasema no pain no gain. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa, tulikuwa tukitukanwa hapa, nchi kubwa ya Tanzania tunashindwa na nchi ndogo ndogo. Leo tumenunua ndege sita na mwakani tunanunua ya saba, wapo watu wanakuja na maneno sijui terrible teen, sijui kitu gani. Hayo ni matango pori na mimi namshauri sana Mheshimiwa Waziri akiinuka hapa aseme maneno ya kitaalam awaambie Watanzania na Waheshimiwa Wabunge wasiwe na wasiwasi, hatuna wasiwasi na Mheshimiwa Waziri Profesa aende akanunue ndege eti zenye wasiwasi. Nina hakika kabisa kwamba akiinuka Mheshimiwa Waziri hapa atatuwekea na kutufungia mjadala huu ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kulisema hilo, naomba pia niishukuru sana Serikali yangu, kwa sababu nimekuwa nikiinuka mara nyingi sana kuzungumzia barabara ya kutoka Mkuranga Mjini kwenda Kisiju - Pwani na sasa kazi imeanza. Nimeona katika hotuba ya Rais ya kwamba upo uwezekano mkubwa mwaka huu tukapata pesa za kutengeneza kilomita mbili za lami, hii ndiyo Serikali ya Awamu ya Tano ya Hapa Kazi Tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwa kuwa barabara hii imekuwa ikitengewa pesa nyingi kila mwaka kwa ajili ya maintenance, tunanunua kokoto zinazotoka Jaribu Mpakani takribani kilomita 65 kufika Mkuranga. Tafadhali sana Mheshimiwa Waziri atazame jambo la namna hii. Waone kabisa kwamba huu mpango waliouanzisha wa lami ya kidogo kidogo waufanye kila mwaka badala ya kuingiza hela nyingi katika maintenance ambayo baada ya muda mfupi inaharibika tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaiona Mkuranga ya viwanda na Mheshimiwa Rais amekuja Mkuranga mara mbili, mwezi huu wa Tano au wa Sita atakuja mara ya Tatu kuja kufungua kile Kiwanda cha Tiles. Mvua hizi za masika zimetaka kukifanya kiwanda kile kisipate malighafi, kwa nini? Kwa sababu barabara ya Kimanzichana mpaka Mkamba, Mkamba - Mkuwili kuungana na wenzetu wa Kisarawe imekufa kwa sababu ya mvua. Naomba sasa tuliangalie jambo hili kwa umakini sana, kwa sababu kiwanda kile kinakwenda kulisha tiles za nchi nzima, hatutakuwa na sababu ya kununua tiles kutoka nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri iangalie hii ni barabara ya uchumi, watu walikuwa wakisema humu kwamba malighafi za kiwanda hicho zinatoka nje ya nchi. Nataka nikuhakikishie malighafi yote inatoka Kisarawe, Kilindi
- Tanga, Mkuranga, Kisegese, Vianzi na Mkamba. Hivyo, naomba barabara hii ifanyiwe kazi maridadi kabisa ili tuweze kuinua uchumi wa watu wetu na watu wetu waweze kuona kwamba utengamano wa viwanda na uchumi wao unakwenda sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kwa ufupi sana nizungumzie suala la kupandishwa hadhi za barabara. Ninazo barabara mbili ningependa zipandishwe hadhi. Barabara ya Kiguza – Hoyoyo, Hoyoyo mpaka kwenda kutokea Kitonga - Mvuti. Barabara hii upande mmoja ni trunk road ya Natioal Road - Kilwa Road na upande mwingine ni barabara ya Mkoa wa Dar es Salaam. Pande zote hizi mbili zinabeba mizigo mizito tena zina lami, lakini sisi barabara yetu ya Kiguza – Hoyoyo kupita pale Hoyoyo kwa Mama Salma pale ni barabara ya vumbi na barabara imechoka. Sasa tunabebeshaje mizigo mikubwa barabara hii na Halmashauri hazina uwezo. Naomba sana Mheshimiwa Waziri akiona barua ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Kamanda Injinia Evarist Ndikilo aipitishe haraka barabara hii nayo pia vilevile iweze kupata kupandishwa hadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hiyo iko barabara ya Vikindu mpaka Vianzi – Marogoro – Sangatini, upande wa Dar es Salaam kutoka Tundwi - Songani, Pemba Mnazi - Kibada - Mwasonga mpaka Kimbiji inawekwa lami. Upande wetu huku kilomita kama kumi bado ni barabara ya Halmashauri inabeba mzigo mzito. Naomba sasa kwa heshima kubwa na taadhima tuendelee kuthibitisha ya kwamba hii ni Serikali ya Hapa Kazi Tu na akiiona barua ya Engineer Evarist Ndikilo, Mkuu wa Mkoa, Kamanda kabisa basi aitie mkono wake pale Mheshimiwa Waziri, ahakikishe kwamba mambo yanakaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba nichukue fursa hii kuipongeza tena Serikali kwa kazi kubwa inayoifanya ya kulipa madeni ya Wakandarasi. Tunaomba pia iendelee kuhakikisha jambo hili linafanyika kwa ufasaha kwa maana liharakishwe na pesa zinazokwenda katika Halmashauri zetu ziharakishwe, tena nafahamu kwamba Serikali ina mpango mzuri sana wa kuanzisha Agency ya Barabara za Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wenzangu hapa wamezungumzia jambo la kwamba agency hii ikiwezekana wapewe TANROADS. Sasa sisi hatutaki kurudi nyumba, tunachosema tutakuja kumwambia Waziri wa Fedha aangalie uwezekano ikiwezekana hii Agency ya Barabara za Vijijini ipate pesa na asilimia kubwa zaidi ya ile ya thelathini. Kwa sababu uti wa mgongo wa wananchi wetu ili kuwatoa katika umaskini ni kuwatengenezea barabara zao. Watu wangu wa Mkuranga wakiboreshewa barabara zao vizuri ambacho ndiyo kipaumbele namba moja cha miundombinu, nina hakika kabisa kwamba, watainuka zaidi kiuchumi na watafanya shughuli zao wenyewe. Leo hii mananasi pale yanaharibika ni kwa sababu barabara ni mbovu za vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kubwa na taadhima naomba nichukue fursa hii kukushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nichukue fursa hii kukushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia mjadala wa hotuba hii ya maji. Nami naunga mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na niwapongeze sana kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya.


Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijajielekeza katika kuwaombea maji wananchi wangu wa Mkuranga, uniruhusu nitumie nafasi hii ya dakika moja, mbili kuwaonesha Watanzania kwamba Chama cha Mapinduzi bado ndiyo Chama imara chenye haki ya kuendelea kuwaongoza Watanzania. Tulipokuwa katika uchaguzi wa East Africa kwenye Bunge hili, hatua ya kwanza Chama cha Mapinduzi kiliwakataa Mheshimiwa Wenje na Mheshimiwa Masha. Wenzetu wakaondoka wakaenda kuwaambia Watanzania kwamba sisi tunataka kuwachagulia watu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jana unafiki wa Vyama vya Upinzani umedhihiri katika Bunge hili. Wale waliowaleta sisi tukawakataa, wametusaidia jana kuwakataa kwa vitendo. Makamu Mwenyekiti wao Profesa Safari wamempa namba ya viatu, namba 35, Wenje wamempa namba 34, Masha wamempa namba 44. Tunaendelea kuwaambia Watanzania kwamba Chama cha Mapinduzi ndicho chama cha kweli na ndicho chama cha kukiamini na Wapinzani hawa ni wanafiki wakubwa! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo na ujumbe umefika, naomba nisema yafuatayo sasa.

UTARATIBU...

MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka tuwaambie sisi bado ni Walimu katika Taifa hili, wao wakijua hivi, sisi tunajua hivi, hiyo ndiyo habari. Nataka nimwambie Mheshimiwa Waitara, rafiki yangu kwamba hiki ndiyo Chama cha Mapinduzi ambacho hata yeye kilimlea pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, jana tumeendelea kuuthibitishia Umma wa Watanzania kwamba hiki ndiyo Chama cha Mapinduzi. Tutaendelea kuwafunzeni siasa, kwa sababu hiyo ndiyo kazi yetu. Kesho tutakwenda kupitisha bajeti ya Wizara ya Maji. (Kicheko/Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, ombi letu ni kutaka kuona kwamba katika bajeti hii ya Wizara ya Maji tozo ya shilingi 50 inaongezeka. Mheshimiwa ukikaa hapo katika kiti tuelekeze, Kamati yetu ya Bajeti ikakae na Serikali iongeze bajeti ile ya tozo ya shilingi 50 tukawahudumie Watanzania. Watanzania wa Mkuranga Mjini wanayo maji pale katika Mlima Kurungu, kisima cha mita 600, kuna maji ya litres nyingi yanapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mtu mmoja pale anaitwa Manyaunyau, anawauzia Watanzania wa Mkuranga maji. Mtu mmoja amechimba yeye binafsi. Katika bajeti ya 2014/2015 zilitengwa hela hazikwenda, mwaka huu wa fedha wa 2015/2016 uliokwisha zilitengwa pesa hazikwenda. Sasa katika bajeti hii tunachotaka pesa ziende. (Makofi)



Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali. Katika miradi ya visima kumi, mimi nimechimba visima kumi Mwanambaya, Mlamleni, Mkenezange, Kimanzichana, Mdimni, Ng’ole, Mbulani, Yavayava, nimechimba huko kote. Ninachosubiri sasa ni kuona miundombinu ya maji inaenea kwa wananchi wa Jimbo langu la Mkuranga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sina wasiwasi kwa sababu nikimtazama jemedari wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, naamini kabisa kwamba maji yanakwenda kutatuka na Watanzania ile nia yetu tuliyowaambia ya kumshusha mama ndoo kichwani, tutaifanya hiyo kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri mimi ni Mbunge mpambanaji.

T A A R I F A....

MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, unilindie muda wangu. Nimesema hapa ya kwamba na sisi hicho alichokisema ndicho tunachokitaka. Hizi pesa zilizotengwa tuhakikishe zinakwenda kwa wananchi. Hizi pesa zikienda, tuna hakika azma yetu ya kumshusha mama ndoo kichwani itakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hapa ya kwamba tuongeze tozo hiyo shilingi milioni 181, ninety something millions zote zimetoka katika tozo ya mafuta. Tukiongeza tuta-double, tutawasaidia Watanzania wakiwemo wa kwa rafiki yangu Mwalimu Marwa kule Serengeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kwa umuhimu kabisa, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri anisaidie kunipelekea pesa zile. Ukurasa wa 163 ziko peza zinapelekwa kwenye Miji 63. Mmoja katika huo Mji uwe ni Mji wa Mkuranga. Sisi hatutaki pesa nyingi, tunataka kama shilingi milioni 800. Nami kwa kuwa ni Mbunge mpambanaji, nimeshajiongeza, nimezungumza na Ubalozi wa Kuwait, wameniambia yatoe maji kutoka mlima Kurungu yapeleke katika tenki. Jenga tenki, sisi tutakusaidia katika pesa za kufanya distribution. Unataka nini tena? Mungu akupe nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa heshima kubwa na taadhima niseme kwamba Mawaziri wetu chapeni kazi, sisi tuko pamoja na ninyi, kazi yenu mnayoifanya tunaiona na tunataka tuwahakikishie mkienda mkakaa Serikali na Kamati yetu, mkatukubalia, tukaenda kubadilisha katika Sheria ya Fedha, tukaongeza tozo ya shilingi 50, basi mambo yatanoga sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata fursa hii ya kuchangia dakika hizi mbili, tatu za mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ya kwangu ni ushauri. Kwanza napenda ni-declare interest kwamba katika fani ambazo nimezisomea ni pamoja na hii fani ya uvuvi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niishauri Serikali yangu, nimshauri Mheshimiwa Rais na kwa kusema ukweli, Mheshimiwa Rais wetu nia yake ni njema sana. Nataka nimwambie kwamba kuna mapato makubwa sana kwenye uvuvi wa Bahari Kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa dunia nzima inahamia kwenye jambo linaitwa blue economy. Naomba niitolee mfano Kisiwa kidogo cha Maldives ambacho kina wavuvi 8,139, sisi tuna wavuvi wadogo wadogo 203,000. Maldives ina vyombo vilivyosajiliwa vya kufanya uvuvi ambao wao wanategemea spicies moja tu ya samaki aina ya tuna, mwenzangu Mheshimiwa Ngwali ametoka kusema hapa, tena amesema kwa kufoka kwelikweli, sisi tuna vyombo vilivyosajiliwa vya maji baridi na maji chumvi zaidi ya 59,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ikiwekeza katika uvuvi, hasa huu wa Bahari Kuu ambao hatujautumia vyema mpaka hivi leo, nataka nikuhakikishie kwamba tutapata kipato kikubwa sana na inaweza ikawa ni sababu ya kuinua uchumi wetu na ajira za watu wetu kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, Mheshimiwa Rais katika mwaka mmoja huu na nusu amenunua ndege za kutosha na anaendelea kutuboreshea, tunajenga SGR, tunajenga flyovers, namwambia Mheshimiwa Dkt. Tizeba mwambie Rais wetu anunue meli ya uvuvi wa kisasa, wa kibiashara. Meli ambayo itachakata na itafanya na mambo mengine yote, utaona namna ambavyo GDP inayopatikana kutokana na uvuvi, Wabunge wote humu tutakuja kushuhudia sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni huo, najua kwa kufanya hivyo, sisi watu wa Mkuranga tutapata sasa matrekta tunayoyalilia. Maana Wilaya nzima ya Mkuranga haina trekta la Serikali hata moja, tuna matrekta 22 katika vijiji 125, yote ni ya watu na yote ni mabovu. Sasa katika uchumi wa namna hii tutapataje lakini tukienda katika blue economy, sisi tumesoma pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Mwalimu wangu, Mheshimiwa Dkt. Sware yule pale na wapo Walimu wangu wengine wengi kule, akina Dkt. Tamatama Rashid na wengineo, hawajatumika ipasavyo katika blue economy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena, Mheshimiwa Dkt. Tizeba na kaka yangu Mheshimiwa Olenasha, mwambieni Mheshimiwa Rais tununue meli ya uvuvi hata moja tu ya Serikali, mtaona namna ambavyo uchumi wa nchi hii utakavyopanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii niliyopata.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nami naomba nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa fursa ya kusema kwenye bajeti hii ya Wizara ya Maji. Nimesimama kuunga mkono hoja, na pili, nimesimama kuchangia kidogo kwenye bajeti hii ya Wizara ya Maji inayoongozwa na Mheshimiwa Aweso.

Mheshimiwa Spika, nami nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, maana mwaka 2022 tulipata mitambo kwa ajili ya uchimbaji wa visima na mabwawa katika mikoa yetu. Kwa kuwa maji haya ni kwa ajili ya wanadamu, lakini pia maji haya ni kwa ajili ya mifugo na huduma nyingine ikiwemo kilimo, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge baadhi ya waliochangia hapa leo, wakisisitiza kwamba, katika maeneo yenye mifugo na ikiwa kama uko mradi wa maji kwenye eneo lile, basi ni vizuri sana ule mradi wa maji uzingatie kutoa huduma kwa mifugo pia.

Mheshimiwa Spika, katika hili namshukuru sana mtu muungwana, mtu mzuri, mweledi, mchapakazi, Waziri Aweso na timu yake yote, kwa hakika tumekubaliana kwamba katika kila designing ya mradi wa maji pale unapopita kwenye eneo la mifugo, basi uzingatie sana kupatikana kwa namna ambayo utasaidia mifugo yetu kuhudumiwa na maji yale.

Mheshimwa Spika, nimemsikia hapa Mbunge wa Ngorongoro, Mheshimiwa Shangai, vilevile nimemsikia Mheshimiwa Shangazi, wamesisitiza sana. Mimi ninafahamu, kwa wadau wa mifugo, sisi wafugaji ni bora wakati mwingine tukose maji sisi wenyewe lakini mifugo yetu iweze kupata maji. Ndiyo maana ninamshukuru sana ndugu yangu, Comred Jumaa Aweso, kwa kuwa tumekubaliana kimsingi ya kwamba tunakwenda kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwenye kusisitiza juu ya jambo hili, ikiwa mtaona kama kuna wasiwasi juu ya ile designing, siyo tu kumfuata kaka yangu, Mheshimiwa Aweso, hata nami nishirikisheni ili kusudi niweze kusukuma kwa pamoja; mimi, yeye na timu zetu, ili wafugaji wetu waweze kupata maji. Maana sote tunafahamu ya kwamba mifugo ni utajiri, na ili iweze kukaa vizuri, ipate malisho na maji.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nachukua fursa hii kukushukuru sana kwa nafasi hii niliyoipata. Pia naomba nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Mheshimiwa Mabula, Katibu Mkuu na Makamishna wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee kabisa, nimpongeze sana rafiki yangu Kamishna Mathew wa pale Dar es Salaam kwa kazi kubwa anayoifanya, halali usingizi, ni kwa sababu ya kuhakikisha migogoro inakwisha Dar es Salaam. Kamishna wangu wa Kanda ya Mashariki, kwa kweli amenisaidia sana katika mgogoro wa vijiji vinne vya Mlamleni, Luzando, Mwanambaya na Mipeko. Amefanya kazi kubwa na natumai kazi hii ataimalizia vizuri hapo mbele. Vile vile, kwa namna ya kipekee, nitambue kazi nzuri anayoifanya Kamishna wetu wa Kanda ya Kusini, kaka yangu Luanda, wote Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichukue fursa hii kurudia tena kusema kwamba kazi hii kubwa wanayoifanya, Mheshimiwa Waziri, tunalo sisi la kujifunza. Kwa sababu Waswahili wanasema, ukiona vyaelea ujue vimeundwa, Mheshimiwa Waziri Lukuvi, kwake yeye kwa kazi
kubwa anayoifanya na Wabunge wote humu tunamsifu, ni kwa sababu tunakwenda kila mahali, tunatatua migogoro na tunafanya vema sana. Hata kwangu Mkuranga migogoro niliyoitaja na mingine ambayo sikuitaja ameifanyia kazi kubwa sana. Namshukuru sana na Mwenyezi Mungu ambariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalo tatizo katika Kijiji cha Dundani na hili ni tatizo la maeneo mengi linalohusu fidia. Wananchi wanazuiwa kwa ajili ya uendelezaji wa ardhi zile kwa ajili ya uwekezaji, ni jambo jema. Tunapenda uwekezaji, lakini sasa inapofika mahali watu wanasubiri jambo kwa muda mrefu sana inafika miaka mitatu, minne, mitano, maeneo yao yanageuka kuwa mapori, hawawezi kuendeleza chochote katika maeneo yale. Hili linakuwa ni tatizo na linawakatisha tamaa sana wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Waziri, yeye ni champion, atusaidie tutoke mahali pa namna hii. Wananchi wanaozuiwa kuendeleza maeneo yao kwa muda mrefu na yanageuka kuwa ni mapori, hawawezi kuvuna nazi zao, hawawezi kulima mihogo pale, hawawezi kufanya maendeleo ya namna yoyote, tuwasaidie. Kama tumeshindwa tutafute namna ya kukaa nao na tuwarejeshee maeneo yao waweze kuendelea na maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka nitoe ushauri ni eneo la upimaji na uendelezaji wa ardhi. Hili eneo lina potentiality kubwa sana, wazo langu ni kwamba, kwanza nawapongeza sana Wizara, wamekubali kuchukua taasisi na makampuni binafsi kuweza kushiriki katika kazi hizi na hili ni jambo jema, ni lazima tubiasharishe mawazo yetu. Hata hivyo, hapa bado liko tatizo, Wizara ya Ardhi mshirikiane vema hasa na wenzetu wa TAMISEMI, uendelevu wa ardhi kwa kutumia kampuni binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanachukua pesa zao lakini mlolongo unachukua muda mrefu sana, hasa mtu akiwa amekopa pesa yake benki kuweza kufanya marejesho haiwezi kuwa kazi nyepesi tena. Kutoka kununua ardhi mpaka kufika kuipima, mpaka kufika kuisaidia Serikali kuwauzia wananchi ili sasa papatikane ardhi iliyoendelezwa, inachukua kipindi kirefu sana. Matokeo yake inawakatisha tamaa, Mheshimiwa Waziri aMheshimiwa Mwenyekiti, amefanya kazi nzuri ya kuweka bei elekezi, maana sasa ardhi ilikuwa inafanya inflation, kila mtu anajipangia anavyoweza tu, sasa tume-control hilo jambo, ni jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, lazima tuwe na ushirikiano ili hii kazi ya kuipima ardhi yetu ya Tanzania kwa kutumia taasisi binafsi iweze kuwa yenye kuvutia, kazi hii ya kupima Mheshimiwa Waziri peke yake hataweza, tutarudia hapa mwaka hadi mwaka hata miaka mia moja, hatutaweza, ndiyo ile nasema lazima tubiasharishe mawazo yetu. Wizara ya Ardhi na Wizara ya TAMISEMI tushirikiane, milolongo, bureaucracy zimekuwa nyingi sana. Ushauri wangu ni huo kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge wote kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, hakika ni nyota wa mchezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ushahidi ni kwamba ameanza na mkakati wa Royal Tour mkakati unaokwenda vizuri na majibu tunayaona. Ameingia na mkakati wa kuhamasisha katika michezo ikiwa ni sehemu ya utalii na mkakati wa hamasa ya michezo umejibu na matokeo tumeyaona Algeria, timu yetu na vijana wetu wamefanya vizuri. Tunawapongeza sana, hatuna tunachowadai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juu ya michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge inayohusu suala zima linalohusianisha juu ya mifugo na hifadhi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumejipanga vema. Moja katika mipango yetu ni kuhakikisha ranch zetu za NARCO tutazitumia vema. wale wafugaji ambao wamekuwa wakihangaika sasa tunakwenda kuziboresha na tunaanza na pale Mkata ili wale wafugaji wanaoondoka katika Bonde la Mto Kilombero tutakwenda kuwapa eneo pale, ili ile mifugo isiadhirike zaidi, iweze kuingia katika eneo hili na iendelee kutoa mchango katika pato la Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutatoka hapo tutakwenda na maeneo mengine ili kuhakikisha kwamba wafugaji wetu waweze kuwa na maeneo na ndio kitakuwa kipaumbele chetu cha kwanza kwa ajili ya aeneo hili la Serikali kwa maana ya ranch zetu.

Mheshimiwa Spika, la tatu, ni jambo maalum ambalo limezungumzwa hapa na Mheshimiwa Hawa Mwaifunga na Waheshimiwa Wabunge wengine kuhusiana na Msomela. Msomela inakwenda vizuri mno, hivi sasa tunavyozungumza tumejenga kituo kizuri cha maziwa na ili kuhakikisha kituo kile kiwe na tija tumehakikisha tumeunda ushirika wa wafugaji na ushirika ule tutakwenda kuwapa ng’ombe bora ili waweze sasa kupiganisha na ng’ombe walioko pale na kusudio letu waweze kukilisha kituo chetu lita 5,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi, vile vile tumeenda kuwafunza namna ya kuwa na mashamba ya malisho yanakwenda vizuri mno. Tatu, tumeimarisha eneo la majosho na mabwawa ya kunyweshea mifugo. Tunayo mabwawa mawili; moja linajengwa na Wizara ya Maji na lingine tunajenga Wizara ya Mifugo na Uvuvi, yanakwenda vizuri na tutahakikisha kwamba yanakamilika ili kusudi watu wote wanaotoka Ngorongoro wanakuja pale Msomela waweze kufanya shughuli zao za uzalishaji wa mifugo kwa usalama. Vile vile, kwa hakika kinakwenda kuwa kituo cha biashara ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuweza kuchangia mjadala huu wa mapendekezo ya bajeti. Nami moja kwa moja napenda nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wetu Dkt. Mpango, lakini pia napenda nichukue fursa hii kumshukuru Naibu wake na timu nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, popo hajafahamika kama ni mnyama ama ni ndege mpaka hivi leo. Hawa wenzetu hata sitaki kuwaita ni vinyonga, naomba niwaite popo. Maana yake hawajafahamika either ni ndege ama ni wanyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo limewashuka! Walijigeuza kuwa ni Mawakili wa wale ambao sisi tumewatuhumu kwamba ni wezi wetu na yule mhusika mkuu amewathibitishia mchana wa leo, ameingia na amekiri mwenyewe kwa kinywa chake kwamba wako tayari kulipa pesa tunazotaka au tunazowadai. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena lile liliokuwa linaonekana kwamba ni jambo gumu la kujenga smelter katika nchi hii amelichukua na amesema wako tayari kujenga smelter katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Afrika, our home land; Afrika ina bahati mbaya, Wapinzani wa Afrika wamekuwa wakitumika na mabeberu miaka yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, UNITA wametumika na mabeberu kuiangamiza Angola miaka yote, wale pia wanatumika na mabeberu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuna kila sababu ya kutamba. Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, eneo la madini ukurasa wa 32 Kifungu cha 35 (a) kinaeleza wazi wazi, “kuweka na kusimamia mfumo thabiti wa kukagua shughuli za migodi.” Ukienda ukurasa wa 34, hiyo hiyo 35(k) utaambiwa…. (Makofi)

TAARIFA . . .

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaliyotokea mchana wa leo hayawezi kupita hivi hivi, lazima kuna watu wahangaike. Yale mambo siyo mchezo mchezo! Wale Wazungu wakimwaga mzigo hata wa trilioni 10, 20 au 50 tu hapa, haya mambo tunayoyazungumza juu ya barabara zetu, juu ya maji, juu ya shilingi milioni 50 katika vijiji, juu ya SGR, juu ya kuongeza ndege nyingine, juu ya maendeleo yote katika nchi hii, tutapaa! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nikwambie tu na Bunge hili pia, Word Bank wametoa ripoti na wame-predict Tanzania is going to be the third fastest growing economy katika Afrika. Itapitwa na Ethopia kwa 8.3 percent; itapitwa na Ghana kwa 7.8 percent; sisi tutakuwa 7.2. Hiyo ndiyo habari. Nataka nikwambie, ukitaka kuyaona hayo, ndiyo maana utaona watu wamekimbia siti zao leo, wametoka mbele wamehamia kule nyuma. Aibu! Eeh, habari hii ni ngumu! Hii habari ni nzito!

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Dkt. Mpango na timu yake msumari huo umeingia! Hatari sana haya mambo! Huyu JPM sio mtu wa mchezo mchezo, watu wanaweweseka, watu wamepoteza uelekeo! Haya mambo siyo ya mchezo mchezo! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi sasa katika bajeti yetu, natoa ushauri ili yale mapato yaendelee kutuimarisha katika uchumi wetu. Dozi imeshaingia, hela za Morena zimepotea, basi tunasonga mbele. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi katika blue economy. Nasisitiza ya kwamba fisheries, kama Ilani yetu inavyoeleza, tunayo nafasi kubwa sana ya kuendelea kukuza kipato chetu kwa kutumia Sekta ya Uvuvi wa Bahari Kuu, tununue meli tuhakikishe kwamba tunachakata na kufanya maendeleo mengine katika Bahari Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichukue nafasi hii pia kuelezea juu ya kilimo. Wapo watu hapa wamesema Serikali hii haishughuliki na kilimo wakija kwetu sisi tunaolima korosho tunaweza tukawapopoa kwa mawe. Sisi tumeambiwa msimu huu wa kilimo, korosho tutapata sulphur bure, mabomba ya kupulizia bure. Ni nani huyo anayeweza kusimama hapa; Serikali imetuondolea zaidi ya tozo tano za kilimo, wewe leo unasimama unasema mambo yasiyokuwa na kichwa wala miguu!

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba sasa, sisi kama Taifa tunapoteza siyo chini ya Dola milioni 110 kwa kupeleka korosho ghafi nje ya nchi. Hiyo tukibaki nayo, tunao uwezo wa kutengeneza kiwanda cha kuchakata korosho na tukaweza kuuza na tukatoa ajira za kutosha. Tuweke mkakati maalum kabisa; ule uliowekwa na Bodi ya Korosho wa kuhakikisha tunatengeneza viwanda vyetu, basi hilo tusiliache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kupoteza wakati, katika bajeti hii nimeona mambo mengi; mojawapo ya jambo nililoliona ni misamaha mbalimbali kwa viwanda vyetu vya ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
The Finance Bill, 2016
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, nilisahau hili la dakika tano lakini nilichokuwa nataka nikizungumze ni juu ya mabadiliko ya sheria hii niliyoitaja hapo hususani kifungu cha 86 na kile kifungu kidogo cha (3) kilichoongezwa. Sheria hii inahusu matumizi ya mashine za kielektroniki. Nimesoma katika mapendekezo katika kifungu kidogo cha (3), yanamtaja mnunuzi kupewa risiti, muuzaji kutoa risiti lakini pia inataja endapo kama mnunuzi hakupewa risiti ile na muuzaji na hakuripoti jambo lile achukuliwe hatua za kisheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nilichokuwa nataka kukizungumza kwa makini kabisa kwanza ni kushukuru kwamba Kamati imeeleza namna ambavyo Serikali imepokea mapendekezo ya kutenganisha vitu hivi vitatu, muuzaji awe na namna yake, mnunuzi awe na namna yake lakini na bidhaa yenyewe, hili jambo bado limekuwa ni pana sana. Napenda Serikali itupe ufafanuzi juu ya bidhaa kwamba mtu anayekwenda sokoni kununua bidhaa za Sh.20,000 na mtu anayekwenda kununua bidhaa za Sh.1,000,000, tuelezwe kinagaubaga juu ya watu hawa ili wananchi wetu waweze kuelewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, watu walipoona mabadiliko haya ya sheria yameandikwa katika vyombo vya habari, huko vijijini kwetu taharuki imekuwa ni kubwa sana. Sisi tungependa tupate kujua na kuelezwa waziwazi lakini tusiishie katika kuelezwa waziwazi, Serikali kwa maana ya Wizara yetu ya Fedha na TRA ni lazima zihakikishe kwamba zinakwenda kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi wetu wawe na uelewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kwamba Mtanzania mzalendo ni yule ambaye yuko tayari kulipa kodi, tena kulipa kodi bila shuruti, lakini haiwezi kuwa kulipa kodi bila shuruti bila wananchi hawa kupewa elimu. Naomba vitengo vyetu katika Wizara ya Fedha na TRA visiwe vya kuzima moto, liwe ni jambo endelevu hadi huu utamaduni wa kulipa kodi uweze kuzoeleka na watu waone kwamba ni wajibu wao na ni haki yao kulipa kodi kila wakati katika kila transaction wanayoifanya. Bila kufanya hivyo, kuwafanya Watanzania kuona kwamba ulipaji wa kodi ni utamaduni wao bado jambo hili litakuwa ni tatizo na wananchi wetu wengi watajikuta wanaingia katika mikono ya sheria wakaenda kufungwa au kulipishwa faini ambazo hawatakuwa na uwezo nazo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, ningeomba wenzetu wa Wizara ya Fedha na TRA waweke utaratibu wa bonus. Nimetazama katika nchi mbalimbali nimeikuta nchi ya South Korea wameweka utaratibu wa bonus ambao umeanza mwaka 2004 na umefanikiwa sana. Wale wauzaji na wanunuzi zile risiti zao wazihifadhi, waweke bonus kwa muuzaji ambaye anaonesha vizuri juu ya utoaji wa risiti na mnunuzi ambaye anaonesha vizuri juu ya risiti zake, hii itasaidia wananchi wetu kuunga mkono zoezi hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nami naunga mkono agenda hii. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO WA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kukushukuru wewe kwa fursa hii, lakini pili nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, mtoa hoja na timu nzima ya Wizara yake ikiwa ni pamoja na Mheshimiwa Waziri Jenista Mhagama na Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Angellah Kairuki na Naibu Mawaziri wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambapo wengi katika waliotoa hoja wamejielekeza katika kuona namna ambavyo sekta ya mifugo na sekta ya uvuvi zinaweza kuwa na mchango chanya katika pato la Taifa lakini vilevile katika kuinua maisha ya Mtanzania mmoja mmoja. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi imejipanga vyema sana katika kuhakikisha kuwa jambo hili la kuinua kipato cha Mtanzania mmoja mmoja linafanikiwa kupitia mifugo na uvuvi lakini vilevile kuwa mchango chanya katika pato kuu la Taifa. Mathalani, hivi sasa pato la Taifa katika upande wa mifugo ni asilimia 7 na upande wa uvuvi ni asilimia 3 na lengo letu ni kuinua na kuhakikisha kwamba asilimia hizi zinaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna gani tutafanya, ni mikakati mizuri tuliyojiwekea. Moja, ni kuhakikisha kwamba tunadhibiti vyema mnyonyoro wa thamani kuanzia katika kumuandaa ng’ombe mpaka kwenda kumchakata ambapo hivi sasa tumehakikisha kuwa kuna viwanda vipya vinavyokwenda kujengwa vya kuchakata nyama ya ng’ombe. Pale Pwani tuna Kiwanda kikubwa cha Tanchoice lakini hapo Morogoro tunacho Kiwanda kikubwa cha Nguru Hills lakini vilevile tupo katika maridhiano na Serikali ya Misri ambapo tutatengeneza kiwanda kikubwa sana pale Ruvu ambacho kitakuwa na uwezo wa kuhakikisha kuwa nyama nyingi inakuwa processed pale lakini vilevile ngozi na mazao mengine ya mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Dawati la Sekta Binafsi ambalo tumelianzisha sisi Wizarani kwetu, tumehakikisha vile viwanda ambavyo vilikuwa vinasuasua tumeviwezesha. Mathalani, katika upande wa nyama Kiwanda cha Chobo pale Mwanza, tumesaidiana na wenzetu wa Benki ya Kilimo, katika kuhakikisha kuwa wanauchukua mkopo wao na kuwasaidia zaidi ili kuwajengea uwezo ambapo kiwanda kilikuwa kinaonekana kuwa kinasuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lkini vilevile upande wa maziwa, tumefanya kazi kubwa ambapo hivi sasa kupitia agizo la Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli limewezesha Kiwanda cha Tanga Fresh kuwa na uwezo wa kutengeneza maziwa ya muda mrefu, tunaita UHT au Long Life Milk. Ndiyo kiwanda pekee katika Taifa hivi sasa kinachotengeneza maziwa lita zisizopungua 40,000 baada ya kuwezeshwa kupata mkopo wa shilingi 12 kutoka katika benki za kibiashara. Vilevile Wizara yetu tumewasaidia Tanga Fresh ambapo sasa wameweza kuchukuliwa mkopo wao huu na Benki yetu ya Kilimo (TADB) ambapo sasa watakuwa na uwezo zaidi hata wa kufikia lita 100,000 kuzi-process kwa siku moja. Hayo ni kwa ufupi katika upande wa mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa uvuvi, jambo kubwa tulilolifanya ni kuhakikisha kuwa tunafufua Shirika letu la TAFICO. Hadi sasa TAFICO inafanya vizuri, imeanza na tumeshapata pesa takribani shilingi bilioni 4.2 kutoka Serikali ya Japan ambazo zinaenda kusaidia katika kununua meli itakayoanza kufanya kazi ya kuvua samaki wetu lakini vilevile inaenda kufanya ushirikiano wa kuweza kupata meli zitakazokwenda kufanya uvuvi katika eneo la bahari kuu. Mchakato wa kupata eneo la bandari unaendelea ambapo tukishapata eneo hilo tukajenga bandari kazi ya uvuvi wa bahari kuu itakwenda kufanikiwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi pia wamezungumzia juu ya sheria na kanuni zetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Ulega.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO WA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kukupa pole nyingi kwa msiba wa ndugu yetu Mheshimiwa Eng. Nditiye.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze katika kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais, mtunukiwa wa tuzo ya juu ya Kiswahili katika nchi yetu, tuzo ya Shabani Robert ambapo wanapewa watu mahususi, watu mashuhuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nitoe pongezi na shukrani nyingi sana kwa Wizara yetu ya Katiba na Sheria, kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba hongera sana na Kamati yetu; kaka yangu Mheshimiwa Mchengerwa, hongereni sana kwa kazi kubwa na nzuri mliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuhakikisha Mahakama inatumia lugha ya Kiswahili ni jambo jema na zuri sana. Wengi wamesema juu ya kuhakikisha tunawasaidia Watanzania ili waweze kupata huduma kwa urahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii mabenki ambayo yanakopesha Watanzania mpaka yale madogo madogo kwa lugha ya Kiingereza “microfinances” mikataba yote wanayopewa ni kwa lugha za Kiingereza. Mama yule anayekwenda kupata mkopo ule anapewa mkataba kwa lugha ya Kiingereza. Mwanzo mliouanza kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu ni mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama haitoshi, huduma zetu za Bima, Uhamiaji na huduma nyingine zote hutolewa kwa lugha ya Kiingereza. Hili ni jambo zuri mlilolianzisha na Kiswahili ni biashara kubwa. Juzi Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati anajibu swali hapa siku ya Alhamisi alisema kwamba Serikali inajielekeza katika kuhakikisha Kiswahili kinakwenda kuwa biashara kubwa katika dunia na hata kufungua vituo. Ikiwa kama Wazungu, Waarabu, Wareno na wengineo wameweza kufungua vituo katika nchi mbalimbali duniani ikiwemo nchi yetu, nasi ni lazima tuanze.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia hofu ya baadhi ya Waheshimiwa Wabunge akiwemo Mheshimiwa Makamba juu ya kwamba Kiswahili bado hakijajitosheleza, ni lazima tuanze. Jambo lolote linahitaji kuanza. Kulikuwa na hofu hapa ya kuhamia Dodoma, kulikuwa na hofu hapa ya kutengeneza SGR lakini sasa tunakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Jambo ni jema, ni zuri, tusonge mbele. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa fursa hii uliyonipa na pia vilevile naomba nichukue fursa hii kuunga mkono hoja na hali kadhalika kuipongeza sana Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia katika Azimio hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa namna ya kipekee sana nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri mwenzangu na wataalam wetu kwa kazi hii kubwa walioifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, na tatu; nimefurahi sana juu ya michango mbalimbali iliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge iliyotoa msisitizo namna ambavyo tutatakiwa tufanye sisi katika Serikali katika kuhakikisha kwamba Itifaki hii tunaitendea haki na kusogeza mbele maendeleo ya sekta mbalimbali zilizotajwa hapa katika kilimo, mifugo na uvuvi vilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa mifugo kwa maana ya afya ya mifugo na uvuvi, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge juu ya Serikali tulivyojipanga. La kwanza, niwatoe hofu kwenye upande wa instrument kwa maana ya sheria upande wa mifugo sheria zipo na tuna competent authority ambayo ni Directorate of Veterinary Service. Hii inatambulika Kimataifa Sheria ya Mifugo Duniani inamtambua yule DVS wetu hapa, anatambulika kabisa kwa mujibu wa taratibu zote za kidunia, Shirika la Afya ya Mifugo Duniani (OIE) linamtambua.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria yetu ya Usalama wa Mifugo kwa maana ya wanyama na chakula cha mifugo ipo siku nyingi sana ni Sheria Na. 17 ya Mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2007 vilevile tukaiboresha 2019 na tuliiboresha tena mwaka 2020 ili iweze kuendana na hitaji la soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwa na Sheria hii ya Afya ya Wanyama, pia tunazo Sheria za Veterinary ambayo tuna Bodi yake na ipo kwa mujibu wa Sheria Na. 16 ya Mwaka 2003 vilevile na Kanuni zake. Vilevile tunayosheria ya Wakala wa Maabara ya Veterinary na yenyewe yote hii ni katika kuangalia afya ya wanyama. Sheria Sura Na. 245 ni ya siku nyingi na yenyewe pia vilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka niwahakikishie kwa upande wa namna tulivyo tupo vizuri kwa maana ya sheria inayolinda afya ya wanyama kwa maana ya mifugo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitaka kuona namna tulivyokwenda vizuri hapa tazama tuna kitengo kwenye eneo hili la afya ya Wanyama, ndio maana katika miaka mitano iliyopita tumefanikiwa kuanzisha na kuzalisha chanjo ambazo hazikuwepo huko nyuma, yote hii ni katika lile lengo la kuhakikisha mifugo yetu inakuwa na afya njema na kuwalinda walaji wetu. Mwanzo tulianza na chanjo mbili; Chanjo ya Mdondo na Chanjo ya Kimeta, hivi leo tumeshafanikiwa kufika katika chanjo saba; tuna Mdondo, tuna Kimeta, tuna Chambavu, tuna ya kutupa mimba, vilevile tuna chanjo ya mapafu ya ng’ombe, tuna chanjo ya mapafu mbuzi na sasa tunakwenda katika chanjo ya Sotoka ya Mbuzi na chanjo ya Kondoo, tukimaliza hiyo tunatengeneza ya Kichaa cha Mbwa. Hizi zote zinahusiano wa moja kwa moja wa mwanadamu na wanyama. Kwa hiyo, akiumwa mnyama na mwanadamu pia vilevile anadhurika, hiyo ni kwa upande wa mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, nataka niwahakikishie na ndiyo maana hata rate yetu ya kulinda mifugo yetu imeongezeka. Mwaka 2018/2019 tuliweka bajeti ya lita 8,000 ya kuogeshea mifugo tukaanzisha ile programu ambayo haikuwepo kwa miaka mingi sana, mwaka 2019/2020 tukaongeza kutoka 8,000 tukaenda 12,000, mwaka 2021 tumeongeza tena kutoka 12,000 mpaka 15,000 liters na mwaka 2021/2022 sasa tunakwenda katika lita 17,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, nia yetu hapa ni kuangamiza kabisa ugonjwa unaosababishwa na mbung’o. Kwa hivyo, yale magonjwa yote yanayosababishwa na mbung’o yaondoke na rate yetu ya kupunguza maradhi haya ni kubwa sana. Tumeshakwenda chini ya asilimia 30 hivi sasa tulichobaki nacho. Kwa hivyo, Waheshimiwa Wabunge unaweza ukaona jitihada za makusudi za kushindana kuhakikisha tunalinda afya ya mifugo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama haitoshi kwa jitihada hizo tulizozifanya pia pamoja na kuchelewa huku kumetupa nafasi ya kujipanga vema, hapa miaka michache iliyopita hatukuwa hata na viwanda vya kuchakata nyama, hatukuwa na viwanda vya kusindika maziwa. Nimemsikia Mheshimiwa Kiswaga hapa akitaja kiwanda cha ASAS ni moja katika mifano mizuri tuliyonayo. ASAS wana sindika maziwa na yanaweza kuuzwa kokote pale duniani, ni vile tu kwamba hizi itifaki ndiyo zimetuchelewesha, lakini niseme kwamba maziwa yao ni mazuri ukiingia leo katika baadhi ya ndege za Kimataifa kama South African Airways unakuta mtindi wa ASAS unaliwa mle.

Kwa hiyo, hii yote ni mipango mizuri tunajipanga katika kujitosheleza wenyewe ndani ya nchi na vilevile kuuza njeya nchi ndiyo maana tuna ASAS tuna Tanga Fresh, tuna Kilimanjaro Diaries na wengineo na viwanda vya kuchakata nyama.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha tunajitosheleza ndani, lakini tunauza na nje ndiyo maana tumefungua masoko kama yale ya Uarabuni tumemuona Prince Crown wa Saudia alipokuja hapa na wamepita katika machinjio zetu kadhaa. Zile machinjio wameziangalia ubora wake. Nataka niwahakikishie kwamba wameridhika sana, wamekwenda Tan Choice - pale Soga wameona, vilevile wamekwenda na Elia foods kule Namanga wameona kazi ni nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa samaki tunayo maabara kubwa na nzuri ya Nyegezi, ile maabara ya Nyegezi ni maabara ya Kimataifa nataka niwahakikishie inapima vimelea vya kibailojia, lakini inapima na vimelea vya kikemikali. Imekubalika Kimataifa na ndiyo maana Samaki wetu wanaweza kuuzwa Ulaya, wanauzwa Asia, wanauzwa kokote pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge maoni yenu ya namna ya kuweza kuboresha tumeyazingatia na ndiyo maana hata katika bajeti hii mialo kadhaa itatengenezwa, pamoja na kulinda afya za walaji wa ndani na kuendelea kulinda soko letu la nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii nami naendelea kuunga mkono hoja azimio hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii naomba pia vilevile nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mashimba Mashauri Ndaki na kwa namna hiyo pia vilevile naomba nichukue fursa hii kuwashukuru Makatibu wetu Wakuu, Ndugu Tixon Nzunda na Dkt. Rashid Tamatamah lakini na watendaji wote katika wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya kipekee niwashukuru wajumbe wa Kamati yetu wakiongozwa na Mwenyekiti Dkt. Christine Ishengoma; lakini vilevile niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wametuchangia kwa kutupa mawazo, fikra na maoni mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, naomba nichukue fursa hii kuwashukuru sana wapiga kura wangu wa Jimbo la Mkuranga kwa kuweza kuendelea kuniunga mkono wakati wote na kuhakikisha kwamba shughuli zinakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Waheshimiwa Wabunge wengi wamejadili na katika mijadala iliyokwisha kupita; la kwanza, limekuwa ni jambo linalohusu uwezeshaji wa wavuvi. Naomba niwaeleze kwamba jambo hili limetamkwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi; lakini pia limetamkwa katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe shukrani za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan na Serikali ya Awamu ya Sita kwa utayari wa kukamilisha ahadi hizi zilizotajwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Wabunge wengi wameonesha wasiwasi, nikianza na Mheshimiwa Mwantumu Zodo, ambaye alieeleza juu ya miradi iliyokwisha kupangwa katika bajeti ya mwaka 2021/2022 na haikutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ile ilihusu vichanja, cold rooms, ilihusu mambo mbalimbali yaliyowahusu wavuvi ikiwemo na zile alizoziita matumbawe feki ambayo sisi tunaita FADS, yaani Fish Aggressive Devices. Nataka nimuhakikishie ya kwamba fedha zote zile zilizoandikwa katika mwaka ule tumehama nazo, ilipatikana changamoto ambayo tumeieleza katika risala yetu iliyosomwa na Mheshimiwa Waziri na ninataka nimuhakikishie yeye na Wabunge wote ya kwamba vile vichanja vilivyosemwa vitapatikana katika vijiji alivyovitaja vya Mkoa wake wa Tanga kuanzia Moa, Mwandusi, Tawalani, hiyo Mkinga yote itapata lakini vitakwenda mpaka kule Mtwara alipoishia kusema Mheshimiwa Tunza Malapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wakae mkao wa utayari waendelee kuwahakikishia wavuvi wetu hasa wakulima wa Mwani na tena kwa umuhimu zaidi mwaka huu tumeongeza si vichanja vile 52 vitakavyotawanyika mkoa wote katika kilomita zote 1400 lakini tumeongeza zaidi. Katika mpango tulionao mpaka mashine za kukaushia Mwani zipo zimeandikwa katika bajeti hii; na moja ya fedha Bilioni 60 zilizoongezeka zitakwenda kufanya kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, lengo letu ni kuongeza thamani ya mazao yetu na katika kuongeza huku thamani wizara imejipanga vyema. Tumepata wadau ambao wapo serious kwa mfano wadau tuliowataja katika risala kama vile DHL tumekwenda kwa pamoja mkakati wetu wa masoko marketing strategy ambapo tunawaomba Waheshimiwa Wabunge tushirikiane kwa pamoja; vile vikundi lengo letu kila kikundi kimesajiliwa, kipate TBS certificate.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia vilevile kiwe na Barcode yake. Mkakati wetu vikundi vyetu hivi viede kidigitali ndiyo uchumi wa Bluu, uchumi wa kidigitali kwa sababu masoko ya nje yamefunguka na yapo moja kwa moja, tunataka tuukate ule mnyororo wa madalali ili mzalishaji aliyeko kule Moa au Tanganyika anayetengeneza dagaa lake, awe na uwezo wa moja kwa moja kulitangaza soko lake na aweze kuuza bidhaa ile pasipo na shaka yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, ili niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge ambao wameonesha kuwa hawana hakika kwamba kama je hizi fedha zitarudi tena au ziliandikwa halafu ndiyo zimepotea, hizi fedha zipo na nataka niwahakikishieni ya kwamba zitakwenda kufanya ile kazi iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu spika, wapo watu waliozungumzia Bima. Nataka niwaambie kwamba bima ya mifugo na bima ya wavuvi tayari kwa kushirikiana na wizara dawati letu la Sekta Binafsi limeshaanza kufanya kazi na ndiyo maana tumepata mikopo, mikopo imepatikana kwa wavuvi wengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naweza kutaja hapa baadhi ya vikundi ambavyo vimeanza kupata mikopo hiyo. Kule Ukerewe ambako Mheshimiwa Mkundi amesema kipo Kikundi cha Bukasiga kimepata mkopo wa zaidi ya Shilingi Milioni 200. Lakini vilevile pale Sengerema kwa maana ya kikundi cha Kasalazi kimepata mkopo wa zaidi ya Shilingi Milioni 300 na kimeanza kufanyakazi hii hapa; pale Kikumbaitale Geita kwa maana ya Chato wamepata mkopo wa zaidi ya Milioni 200; na kule Kigoma Katonga wamepata zaidi ya Milioni 100; pale Kigoma tena Ujiji kwa maana ya kikundi cha Sangara Beach Amcos kimepata zaidi ya Milioni 70; kwa hivyo, tukichukua fedha hizi za TADB na mkakati tulionao wa hivi fedha tulizopata kwa jitihadi kubwa iliyofanywa na Serikali yetu ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, nina hakika kwamba sasa kazi yetu itakwenda kuwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia, unaweza ukaona Wabunge wengi wameshauri kwa sababu kila mmoja anaona namna ambavyo stock inapungua katika maji yetu ya asili; na kwa hivyo tuna umuhimu mkubwa wa kuwekeza katika ufugaji wa Samaki na ndiyo maana Serikali imedhamiria kuwekeza katika kuwa-train vijana na wale vijana wote wanakwenda kuwezeshwa kupata mikopo isiyokuwa na riba kupitia Benki yetu ya Kilimo ya TADB kupitia hizi fedha zilizoongezeka ambazo ni takriban Bilioni 60; kwa hivyo, tutakuwa na vituo atamizi zaidi ya 200 katika maji ya Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanzia tumeona tuanze huko kwa kuwa utafiti umekwishakufanywa na uwezeshaji sasa utakwenda kuwezesha vizimba zaidi ya 900 ambavyo vitakwenda kuwaajiri vijana zaidi ya 1500.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge naomba mtuunge mkono kwa sababu kazi kubwa na nzuri inakwenda kufanywa. Baadhi yenu hapa mmetushauri juu ya kwa nini mavuvi bado ni ya kienyeji? Program yetu inakwenda kuwezesha kununuliwa kwa boti zaidi ya 320, zitakazokwenda kuenea baharini kote kule, hizi boti ni za kisasa zitakuwa na fish finders, GPS, na tayari TAFIRI wameshafanya hii kazi, kazi ya kujua wapi Samaki wanapatikana na program imeshatengeneza tunaita PFZ kwa maana ya Potential Fishing Zones. Kwa hivyo, naomba muwe na Imani na muhakikishe ya kwamba tunaungwa mkono katika bajeti hii na kwa kweli kabisa mambo haya ya Uchumi wa Bluu sasa yanakwenda kufanyiwa kazi. kwa upande wa mifugo pia vilevile kwa ufupi sana tumejipanga na tutakuwa na atamizi za vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulianza hii kazi pale Kongwe TARIRI. Kwa mumalizia naomba kwa heshima kubwa na taadhima Waheshimiwa Wabunge muendelee kutuamini, mtuunge mkono, mtupitishie bajeti yetu hii na Inshaallahu Taallah nawahakikisha ya kwamba kazi hii kubwa na nzuri inakwenda kufanywa. Ahsanteni. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo, wa Mwaka 2016
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa fursa hii. Nami moja kwa moja naomba nijielekeze kwanza kwa kuwapa pole wenzetu wa kule Bukoba kwa maafa yaliyotokea ya tetemeko la ardhi na Mwenyezi Mungu awalaze mahali pema peponi wale wote waliotangulia mbele ya haki, lakini awaponye kwa haraka zaidi wale wote ambao hivi sasa wamekuwa wakiugua maumivu mahospitalini na adha mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nichukue fursa hii pia vile vile kuipongeza sana Serikali yetu kwa kuleta sheria hii inayohusu Taasisi zetu za Utafiti wa Kilimo na Taasisi ya Utafiti Uvuvi. Imekuja wakati muafaka katika kuwasaidia watafiti wetu kuhakikisha kwamba wanaifanya kazi yao vizuri kwa maendeleo ya Taifa letu na kwa maendeleo ya dunia yetu kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazo angle mbili, tatu ambazo ningependa nizizungumzie katika sheria hizi. Nitayazungumza mambo yote mawili kwa pamoja yanayohusu uvuvi lakini pia vile vile nitayazungumza mambo yanayohusu kilimo. Kabla sijakwenda katika kuzungumzia uvuvi na kilimo, nataka nitoe ombi hasa kwa wenzangu, maana unasikia hapa, watu wanajadili Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo, mwingine anaanza kuzungumzia mambo ya Polisi na UKUTA, anaacha kuzungumzia masuala yanayohusu utafiti wa uvuvi kwa kuwa hana jambo anaenda kuzungumzia jambo linalohusu nyanya zake kule Kilombero zimepondeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ni wakati muafaka watu kama hawa, rafiki yangu Mheshimiwa Lijualikali, jamani mtusaidie tupate elimu ya kujua hivi vitu vya kwenda kujadili. Hili jambo linahusu utafiti! Bahati njema sana katika sayansi hakuna blah blah! Sayansi inazungumzia facts! Sasa mimi nataka nitoe elimu inayohusu facts na siyo blah blah!
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisikia Yalaah, ujue imempata huyo! Ehee! Kwa hiyo, usishituke, imewapata hiyo! (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuishauri Serikali juu ya suala hili linalohusu utafiti, kwanza, tuhakikishe kwamba COSTECH ndiyo inayopelekewa pesa na baadaye taasisi zetu zinakwenda kushindania pesa kule COSTECH. Jambo lililokuwa la msingi hapa ni kuhakikisha kwamba COSTECH wanaweka vipaumbele sawa na watu wote wanavyohitaji, maana Taasisi ziko nyingi. Inawezekana kwamba Taasisi nyingine zisipate pesa hizo kutoka COSTECH.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, jambo la msingi hapa ni kuhakikisha kwamba ili kila taasisi iweze kupata zile pesa, wakati mwingine taasisi zetu za uvuvi na kilimo hazipati kabisa hizo pesa, kwa sababu COSTECH inakuwa kwamba, hawa watu wa uvuvi na kilimo labda hawakuingia katika ushindani wa zile pesa ambazo zinagombaniwa kule COSTECH. Kwa hiyo, ni jambo la msingi kwamba COSTECH wajitahidi kuweka utaratibu ambao utasaidia taasisi zetu zote zihakikishe zinanufaika na pesa hizi za walipa kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi kirefu sana, taasisi zetu zimekuwa zinategemea pesa za wafadhili, ambapo maana yake ni nini? Ni kwamba Donor anayeleta pesa zile, analeta kufuatana na kile anachokitaka yeye. Anayelipia zumari, ndiye anayechagua nyimbo. Sasa ni jambo la msingi kuhakikisha tunaongeza nguvu kule COSTECH na kuipa utaratibu mzuri ili taasisi zetu hizi tunazozitungia sheria leo ziweze kunufaika na pesa za Watanzania badala ya kutegemea zile pesa za Donors tu peke yake. Tukitegemea pesa za Donors peke yake, matokeo yake ni kwamba tafiti nyingi hazitafanyika na hivyo matatizo mengi yanayotokana na kutokufanyika kwa tafiti yatajitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kulisema hilo, nataka nizungumzie jambo la vifaa vya uvuvi. Kwa kipindi kirefu sana tumeona kwamba yanatokea matatizo mengi katika maziwa na bahari kwa ajili ya vifaa vya uvuvi, lakini sheria haijataja juu ya kutafiti ni vifaa gani hasa vilivyokuwa bora. Tunafahamu kwamba wakati wote imekuwa ikizungumzwa size ya nyavu kwamba size hii ndiyo inayofaa zaidi, lakini tungefurahi kuona kwamba sheria inataja na hivi vifaa vya uvuvi viweze kufanyiwa utafiti ili viendane na hali halisi ya kimazingira na wakati vile vile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumza ni database. Tumefanya tafiti nyingi sana, nami nawashangaa wale ambao wanasema kwamba tunatunga sheria hizi za tafiti hazitusaidii kitu. Leo nataka nikuhakikishie, bila hizi tafiti hata hii jeuri ya kusema kwamba hakuna kilichofanyika na hazina faida hizi tafiti, watu wasingekuwa nayo. Hata hivyo wanasayansi tunafahamu kwamba hizi tafiti ni muhimu na hii sheria bado ni muhimu, cha msingi ni kuhakikisha tunakuwa na database ya tafiti zetu zote tulizozifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi tafiti kama hazikutusaidia leo, zitasaidia vizazi vyetu; ndiyo maana ya elimu! Elimu haishii kwamba itatusaidia leo. Watoto wetu kule mbele watakapokuwa wanakwenda kusoma, wataona kwamba sisi huko nyuma tuliwahi kufanya utafiti wa jambo kadha wa kadha na limewekwa mle katika archives au vinginevyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho nililokuwa nataka nilizungumze la kuishauri Serikali, najua lipo katika mipango yetu, lakini mipango iliyopo ni ya kiuchumi juu ya bandari ya uvuvi. Uwepo wa bandari ya uvuvi utasaidia pia watafiti wetu. Unapokuwa na bandari ya uvuvi maana yake ni kwamba watafiti wetu wanapokwenda kufanya shughuli zao za utafiti wanapata mahali pa kuweza kutia nanga na hatimaye kutoa results za utafiti wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, nashauri sheria itaje juu ya muda wa ufanyikaji wa tafiti. Wadau wanalalamika sana; wapo watu wanapewa nafasi ya kufanya utafiti kwa miaka tisa...
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.8) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia. Nashukuru kwa michango ya Waheshimiwa Wabunge waliochangia na nimezisikia hoja zao, lakini kwenye muswada huu kifungu hiki cha 21 sisi tumeboresha sheria mama. Ukisoma sheria mama ambayo ni Sheria ya Uvuvi namba 22 ya mwaka 2003 kuanzia section number 8(3)(a),(b),(c) na kipengele cha 4 ambacho sisi sasa ndio tumekiboresha tayari vifungu vyote hivi vilishatoa huu uelekeo. Hapa kuna maboresho madogo.

Waheshimiwa Wabunge ni kwamba sheria mama ilikuwa tayari inatupa sisi mamlaka toka hapo mwanzo. Ukisoma kifungu cha 3 na 4; kifungu cha 3 tayari kimemtaja Mkurugenzi na mamlaka yake ya kuisimamia sekta ya uvuvi katika maeneo yote ya nchi yetu na ku-oversight namna ya shughuli za usimamizi na ulinzi wa rasilimali tayari imetaja. Tulichokifanya sisi katika maboresho haya ni kwamba kile kifungu cha 4 ambacho ndio tumekirekebisha tumeongeza mambo kadhaa na mambo yenyewe mwanzo Waziri wa Uvuvi alikuwa hawezi kuchukua hatua hata unapokuwa uvuvi haramu umekithiri katika eneo lile na ikumbukwe kutokana na utaratibu wetu wa D by D asilimia 80 ya shughuli zote za uvuvi zinasimamiwa na Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sisi tukasema kwa kuwa jambo hili limeonekana halifanyi vizuri tukampa meno Waziri wa Uvuvi achukue hatua, akishamaliza kuchukua hatua ndio sasa atawasiliana na Waziri wa TAMISEMI washauriane juu ya nani atakayesimamia shughuli ile na hapa kuna options mbili. Ya kwanza atakayesimamia atakuwa ni jirani yake kwa mfano Halmashauri ya Ukerewe jirani yake na ikijuonekana kwamba yuko mbali atakayesimamia itakuwa ni Wizara na katika sheria hiyo sheria mama maana Mheshimiwa Makamba alisema kwamba je, mapato ya Halmashauri ile inayonyang‟anywa yanakwenda wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria mama kifungu kidogo cha 6 kinaeleza wazi iko hapa ni nani atakayesimamia hayo mapato na sisi hatujaigusa ile ya nani atakayesimamia mapato iko vilevile katika sheria mama. Kwa hiyo, kimsingi hapa maboresho tuliyoyafanya ni kumpa meno Waziri wa Uvuvi aweze kuisimamia sekta vizuri ili kusudi Halmashauri ambazo zinaonekana suala hili kwa mfano Halmashauri ya Ukerewe over 90% ya mapato yake yanatokana na shughuli ya uvuvi, lakini angalia ni kiasi gani ambacho wanakirudisha kwenda kusimamia hiyo shughuli ya uvuvi utakuta kwamba ni kiasi kidogo sana au hakuna kabisa. Kwa hiyo, hiii ndio hoja ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili lile la fines naomba niwaeleze Waheshimiwa Wabunge kwamba katika sheria mama kifungu cha 47 kili-generalize mvuvi mdogo kabisa na yule mzalishaji wa nyavu kiwandani au mwenye kiwanda cha ku-process minofu wote walikuwa wanachukuliwa na sheria moja hiyo hiyo. Sasa tunadhani kwa sheria ile ya shilingi 100,000 mpaka 1,000,000 hawa wahalifu wakubwa tumekuwa tukiwakosa, watu wanaingiza samaki wenye sumu makontena na makontena, lakini akiingia unakwenda na sheria hii namba 47 faini yake ni shilingi 100,000 hadi 1,000,000. Kwa hiyo, matokeo yake sisi kama Taifa tunapata hasara, ndio maana tukasema tugawanye ndio tukaja sasa na sheria hii ya amendment namba 23 ambayo Mheshimiwa Makamba alileta clause ile ya kwamba tuiondoe, tukasema tu-categorize tuweke mafungu mawili; wale wahalifu wakubwa na wahalifu wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wahalifu wakubwa tukasema watapigwa faini isiyopungua milioni 10 mpaka milioni 50 isizidi hawa ni mapapa, wanaozalisha nyavu ambazo zinaenda kuwaumiza wavuvi wadogo. Hawa wadogo tukasema watalipa shilingi laki mbili na isizidi milioni 10 ndio sheria hii hapa namba 47 mapendekezo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Naibu Waziri kwenye hilo ungeliwasaidia tu kusoma kifungu cha sheria kuhusiana na faini vinavyosomeka sasa hivi.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, kifungu cha sheria mama, kinasema kama ifuatavyo kwa ruhusa yako naomba kunukuu; “ Any person who contravenes the provisions of this Act other than those who specify penalties, upon conviction should be liable to a fine of not less than 100,000 shillings and not more than 1,000,000 shillings.” Ime-generalize wote ndiyo tukasema tu-categorize kwa sababu hapa kuna kundi kubwa la wahalifu tunalikosa ambalo ndilo linawafanya wavuvi wetu wadogo waingie katika makosa haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo katika consultation, mimi na Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika ile sheria ya kwanza namba 21 kimsingi tumekubaliana. Mwanzo sheria mama ilikuwa inataka mimi nifanye consultation na Waziri wa TAMISEMI, lakini jambo hili lime-prove failure. Sasa tukaamua sisi tuta-suspend, tukishamaliza ku-suspend zile shughuli tutawasiliana na Waziri wa TAMISEMI tukubaliane ni nani atakayesimamia shughuli zile baada ya kuwasiliana na Mwanasheria Mkuu wa Serikali tumekubaliana tuiboreshe kidogo. Kabla ya ku-suspend Mwanasheria Mkuu wa Serikali analeta amendment kwamba mimi nitam- notify Waziri wa TAMISEMI juu ya nia yangu ya kusimamisha Halmashauri ile inayoonelana haifanyi vizuri.