Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Kunti Yusuph Majala (7 total)

MHE. KUNTI Y. MAJALA Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka walimu wa kike katika Shule za Msingi Birise na Donsee ambazo hazina walimu wa kike?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, asante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya ukosefu wa walimu wa kike katika Shule ya Msingi Birise na Donsee zilizopo katika Halmashauri ya Chemba, Mkoa wa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto hiyo Halmashauri ya Wilaya ya Chemba imempeleka mwalimu mmoja wa kike katika Shule ya Msingi Donsee wakati ikiendelea na utaratibu wa kukamilisha kumpeleka mwalimu mwingine wa kike katika Shule ya Msingi Birise.

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali ikijiandaa na mpango wa ajira na mgawanyo wa walimu wapya kwa Halmashauri zote nchini, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inazielekeza Halmashauri zote nchini kufanya msawazo wa walimu wa shule za msingi na sekondari kwa kuzingatia jinsia.
MHE. KUNTI Y. MAJALA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itasambaza umeme katika Kata za Handa, Lalta, Sanzawa na Mpendo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yussuf Majala, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji ambavyo havijapata umeme katika Wilaya ya Chemba vikiwemo vijiji vya Kata za Handa, Lalta, Sanzawa na Mpendo vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili ulioanza kutekelezwa mwezi Machi, 2021 na utekelezaji wa mradi huu utakamilika ifikapo Desemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za mradi kwa Wilaya ya Chemba zinajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 umbali wa kilomita 681.4, msongo wa kilovoti 0.4 umbali wa kilomita 50, ufungaji wa transfoma 50 za 50kVA, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali wapatao 1,100 kwa gharama ya takriban Shilingi Bilioni 27.3.
MHE. KUNTI Y. MAJALA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua changamoto kubwa ya maji inayowakabili wananchi wa Mji wa Chemba?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, Kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yussuf Majala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya huduma ya maji inayowakabili wananchi wa Mji wa Chemba ambapo kwa sasa hali ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama ni chini ya asilimia 50. Katika kutatua changamoto ya huduma ya maji katika mji huo, Serikali ina mpango wa muda mfupi na mpango wa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika katika mpango wa muda mfupi, kazi zilizopangwa kwa ajili ya kuboresha huduma ya maji katika mji huo kwa mwaka wa fedha 2021/2022 ni pamoja na ujenzi wa matanki mawili ya kukusanya maji ya ukubwa wa lita 50,000, nyumba ya mitambo ya kusukuma maji, ununuzi na ufungaji wa pampu nne (4), ununuzi na ulazaji wa mabomba ya umbali wa kilometa 11.6. Kukamilika kwa kazi hizo kutaongeza uzalishaji wa maji kutoka wastani wa lita 50,000 kwa siku hadi lita 320,000 kwa siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali ilipata mkopo kutoka Serikali ya India kupitia Benki ya Exim India jumla ya Dola za Marekani millioni 500 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi katika miji 28 nchini ukiwemo Mji wa Chemba. Maeneo yatakayonufaika katika utekelezaji wa Mradi huo ni pamoja na Paranga, Makamala, Kambi ya Nyasa, Gwandi, Chambalo na Chemba yenyewe. Ujenzi unatarajiwa kuanza wakati wowote katika mwaka huu wa fedha 2020/2021 na umepangwa kutekelezwa kwa miezi 24.
MHE. KUNTI Y. MAJALA aliuliza: -

Je, lini Serikali itamaliza kulipa fidia Wananchi wa Makole waliopisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege na Mkonze waliopisha ujenzi wa SGR?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yusuph Majalla, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya ndege Tanzania (TAA) imekamilisha malipo ya fidia kwa wananchi kutoka kaya 14 za Mtaa wa Chaduru B, Kata ya Makole, Dodoma Mjini, zilizopisha upanuzi wa Kiwanja cha Ndege Dodoma. Fidia hiyo, iligharimu kiasi cha shilingi 1,900,000,000, ilihusu upanuzi wa kiwanja kwa mita 150 zilizohitajika. Serikali haitahitaji kupanua zaidi Kiwanja cha Ndege cha Dodoma kwa kuwa imeanza kujenga Kiwanja cha Ndege cha Msalato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) imekamilisha tathmini ya fedia kwa wananchi wote wa Mkonze ambao maeneo yao yatatwaliwa kwa ajili ya ujenzi wa SGR. Zoezi la ulipaji wa fidia lilianza kufanyika kuanzia tarehe 4 Aprili, mwaka huu 2023. Naomba wananchi ambao bado hawajalipwa wawe na subira wakati zoezi la malipo likiendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, naomba kuwafahamisha Waheshimiwa Wabunge kuwa, ujenzi wa reli ya SGR unafanyika kwa utaratibu wa Sanifu na Jenga (Design and Build), hivyo utwaaji wa maeneo ya nyongeza utaendelea kufanyika kwa kadiri ya mahitaji, kwa mujibu wa sheria, na taratibu za nchi, ahsante.
MHE. KUNTI Y. MAJALA aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kupeleka walimu wa kike katika shule za sekondari na msingi – Chemba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA YA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitoa ajira ili kukabiliana na upungufu wa walimu shuleni unaotokana na walimu kustaafu, kuacha kazi, kufukuzwa, kufariki na ongezeko la idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa. Kwa mwaka 2021/2022 Serikali imeajiri jumla ya walimu 26,598 wakiwemo 16,640 wa shule za msingi na 9,958 wa shule za sekondari.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa ajira zilizotangazwa 2021/2022, Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ilipata Walimu 46 wa kiume na Walimu 49 wa kike kwa shule za msingi na sekondari.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI imetoa maelekezo kwa Makatibu Tawala wa Mikoa yote Tanzania Bara kufanya msawazo wa Walimu kutoka shule zenye ziada na kuwapeleka katika shule zenye upungufu zaidi kwa kuzingatia jinsia ili kuwa na uwiano wa Walimu wa kike na kiume kwenye shule zetu mbalimbali.
MHE. KUNTI Y. MAJALA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa fedha za ujenzi wa stendi ya Wilaya ya Chemba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba kuwa na Stendi ya Mabasi na kwa kuzingatia umuhimu huo tayari imetenga eneo lenye ukubwa wa ekari 22 na tathmini ya gharama za ujenzi wa stendi hiyo ni takribani milioni 643.82.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuanza na kukamilisha stendi hiyo, Halmashauri ya Wilaya ya Chemba inashauriwa kuandaa andiko la mradi huo ili liweze kutumika kutafuta fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa mradi huo kutoka vyanzo mbalimbali vya fedha.
MHE. KUNTI Y. MAJALA aliuliza:-

Je, nini chanzo cha ugonjwa wa manjano kwa watoto wachanga?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tafiti nyingi zimefanyika Kitaifa na Kimataifa kujua chanzo cha watoto wachanga kugeuka njano mara baada ya kuzaliwa. Tafiti hizo zimeonesha kuwa hali ya umanjano hutokea ndani ya masaa 24 baada ya kuzaliwa inaonyesha tatizo la kiafya na linahitaji kutambua sababu na kutoa tiba stahiki.

Mheshimiwa Spika, tatizo hili likitokea baada ya masaa 24, mara nyingi linatokana na sababu za kawaida za mwili wa mtoto kupunguza chembechembe nyekundu nyingi alizokuwa nazo tumboni kwa mama, hata hivyo hili pia uchunguzi wa kina ni muhimu ili kujihakikishia.

Mheshimiwa Spika, suala la utafiti ni muhimu na ni suala endelevu katika tiba.