Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji (209 total)

MHE. MASOUD ABDALLA SALIM: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza kwa Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Spika, la kwanza, ni aibu na fedheha kwa Serikali kwa jinsi ilivyowatelekeza wastaafu wake. Ukiangalia nchi ya Kenya na Rwanda, wastaafu wana hali nzuri. Serikali mmepandisha pensheni kutoka shilingi 50,000/= mpaka shilingi 100,000/=, wastani wa shilingi 3,300/= kwa siku, fedha ambayo hata chai haitoshi! Serikali inasemaje sasa? Kuna mkakati wa ziada angalau kuwaongezea pensheni wastaafu kwa shilingi 250,000/= kwa mwezi? Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Spika, la pili, kwa mujibu wa Ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, miaka kadhaa, miaka mbalimbali, imekuwa ikiripoti kupunjwa, kudhulumiwa kwa mafao ya wastaafu na Serikali imekuwa ikisema kwamba wataalamu wake ndio wanaokosea. Tunataka tuelewe, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuweza kutoa mafao stahiki kwa wastaafu wetu?
Pale ambapo wastaafu wanafariki, Serikali imekuwa ikitoa risala za kutoa machozi na kulia, uwongo mtupu! Tabia hii mbaya lini mtaacha? (Kicheko/Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba niseme, siyo sahihi kwamba imekuwa ni fedheha kwa Serikali. Kama nilivyojibu kwenye majibu yangu ya swali la msingi ni kwamba tumekuwa tukiongeza kiwango hiki cha pensheni kwa wastaafu kulingana na uchumi unavyoimarika na tumekuwa tukiliangalia kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mkakati wa wazi wa kuongeza shilingi 250,000/= kwa mwezi kama pensheni; kama nilivyosema mwanzo, tunaangalia kiwango cha uchumi wetu, uchumi utakakaa vizuri kuturuhusu kulipa shilingi 250,000/= tutalipa hiyo shilingi 250,000/=.
Mheshimiwa Spika, kuhusu mkakati wa kutoa mafao sahihi kwa wastaafu kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge katika swali lake la pili; naendelea kusisitiza kwamba uchumi utakapokuwa umeimarika vizuri; na kama mlivyoona kwa speed ya Serikali ya Awamu ya Tano, tunakusanya mapato kwa kiasi kikubwa na tunatarajia kuongeza tax base ya kukusanya kodi ambayo tunazingatia. Moja ya watu wa kuwaangalia ni Wastaafu wetu, wamelitumikia Taifa na tuna uhakika tutaweza kuwahudumia. (Makofi)
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa kuwa, ulipaji wa kodi ili kuiwezesha Serikali kuweza kutoa huduma nzuri kwa wananchi ni wajibu wa kila raia wa nchi hii na kwa kuwa kumekuwa na matatizo mengi katika mfumo wa ulipaji wa kodi katika Serikali Kuu na Halmashauri, kodi usumbufu mkubwa kwa walipa kodi. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mfumo wa ulipaji kodi ili uwe wazi zaidi na kuwawezesha wananchi kuweza kulipa kodi zile zinazotakiwa kulipwa?
Mheshimiwa Spika, pili, kwa kuwa wananchi wengi hawajui umuhimu wa kulipa kodi, je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kwa wananchi na hasa walipa kodi ili waweze kuzijua aina zote za kodi na kuweza kulipa kama inavyotakiwa.ambazo zimekuwa zikileta
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameuliza mpango gani wa kurekebisha mfumo wa ulipaji kodi. Sasa hivi kama mlivyoona na kwa kaulimbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano ya „SASA KAZI TU‟ tumeimarisha mfumo wa ulipaji kodi kuanzia katika ngazi ya Taifa mpaka Halmashauri zetu na mmeona jinsi ambavyo sasa tunaweza kukusanya kodi kwa kiasi kikubwa.
Pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea kuimarisha na Mamlaka yetu ya Mapato Tanzania imejipanga vizuri kuhakikisha kwamba hilo linafanyika katika ngazi ambayo wanafanyia kazi wao na pia mpaka Halmashauri zetu kule wanakokusanya uimarishaji wa ukusanyaji kodi utakuwa wazi kabisa na kila mmoja ndani ya Halmashauri mwenye jukumu hilo anayafanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuhusu kutoa elimu, mpaka sasa hivi tayari tuna kitengo cha utoaji elimu ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania na elimu hii huwa inatolewa moja kwa moja kupitia televisheni zetu mbalimbali tuna vipindi ndani ya wiki na pia utoaji huu wa elimu ya kodi pia hufanywa kwa semina mbalimbali na warsha zinazofanywa na watoa elimu wetu kutoka Mamlaka ya Kodi Tanzania.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba Serikali imebaki katika kuweka mazingira mazuri, lakini naona kwamba mazingira mazuri hayo si kweli sana kwa sababu hayaonekani maana wananchi wanalalamika sana. Kwa sababu ukienda Bureau de Change hii ina rate hii, ukienda Bureau de Change nyingine ina rate tofauti na zimetapakaa sehemu zote kama sisimizi. Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha rates hizo zinalingana? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kuwa Serikali imejitoa katika biashara hii ya kumiliki Bureau de Change lakini huo ulikuwa ni uamuzi wa zamani na tujue kwamba sasa hivi dunia imebadilika, ni dunia ya sasa. Je, atakubaliana nami kwamba sasa umefika wakati wa Serikali kumiliki huduma hii ili kuwaondolea wananchi wake matatizo ambayo wanakabaliana nayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru kwa kuuliza maswali mazuri ya nyongeza ambayo yanakidhi haja na yanaakisi kinachoendelea katika maduka yetu ya kubadilisha fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, jibu la swali lake la kwanza kwamba rates ni tofauti sana kutoka duka moja kwenda duka lingine, nakubaliana naye na hii yote ni kuonesha kwamba tuko ndani ya soko huria na kila mtu anatakiwa ku-charge anavyoona inafaa. Pia kiuchumi, sisi wachumi tunafahamu kwamba bei ya bidhaa yoyote ile hutegemea na demand na supply. Kwa hiyo, kama demand ya bidhaa hiyo ni kubwa bei zitakuwa tofauti kutoka kwa muuzaji mmoja kwenda kwa muuzaji mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, Serikali iweze kurudi kwenye kuendesha biashara kama hizi na kwamba huo ulikuwa ni uamuzi wa zamani, naamini uamuzi ule ulikuwa ni sahihi na bora. Kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba tangu mwaka 1991 Serikali ilishajitoa kuendesha mabenki haya. Tunaendelea kusisitiza, sisi kama Serikali tutaendelea kutunga sera na sheria mbalimbali za kusimamia maduka haya ili yaweze kutoa huduma zilizo bora kwa wananchi wetu.
MHE. CONCHESTER L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Msingi wa swali langu ni malalamiko ya wastaafu wanaopokea pensheni kwamba hawajawahi kuongezewa fedha hizi. Kwa kuwa kuna malalamiko hayo na kwa kuwa Serikali sasa imetoa tangazo hili kupitia swali langu, je, inasema nini kuhusu wale wastaafu ambao hawajalipwa kiwango hicho kipya na wanaelekezwa vipi namna ya kudai fedha zao hizo pamoja na arrears? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa swali zuri la Mheshimiwa Rwamlaza. Alichokisema na Serikali inafahamu kipo, lakini naomba niseme yafuatayo:-
Katika ongezeko hili ni Mfuko wa PSPF pekee ambao umeweza kulipa sh. 100,000 kwa mwezi mpaka leo. Mifuko mingine iliyobaki kwa mujibu wa vifungu vya 25 na 36 vya Sheria ya Mamlaka ya Usimamizi wa Hifadhi ya Jamii Na. 8 ya mwaka 2008 kama ilivyorekebishwa na Sheria Na. 5 ya mwaka 2012, kima cha chini cha pensheni kwa mifuko yote inatakiwa kupandishwa na Mamlaka hii ya SSRA. Kwa sasa Mamlaka hii inamalizia kufanya actuarial valuation kwa Mifuko yote hii na Bodi za Mifuko hii pia zipo katika mchakato baada ya actuarial valuation kukamilika ili waweze kuanza kulipa rasmi.
Mheshimiwa Spika, kuhusu kulipa arrears zao, wastaafu wote watalipwa arrears zao baada ya actuarial valuation kukamilika na Bodi za Mifuko hii kukamilisha mchakato huu kuanzia Julai 2015. Kwa hiyo, wasiwe na wasiwasi watalipwa arrears zao zote.
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru. Pamoja na majibu ma… yasiyoridhisha sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kumekuwa na malalamiko mengi sana ya hawa wastaafu. Mmetutangazia kwamba hapa kazi tu, unaweza ukatuambia ni lini hawa wastaafu watapewa hizo hela kwa sababu sasa ni muda mrefu umepita? Tunataka tupate muda kwa sababu kwa kweli wanakuja kwenye maofisi yetu na wanatusumbua. Naibu Waziri ametangaza kwamba wamelipwa lakini hawajalipwa wakati waliahidiwa? Ni lini sasa Serikali hii ambayo inasema hapa kazi itatoa hizo pesa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Peter Msigwa kwa swali zuri lakini kwa kukiri japo ameishia njiani kwamba kwa majibu yangu mazuri, nakushukuru sana. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, nimesema kwamba bodi hizi zinaendelea na mchakato ili waweze kutangaza baada ya SSRA kumalizia actuarial valuation. Leo hii mchana nitakuwa na kikao na Mkurugenzi Mkuu wa SSRA kuhusu suala hili. Naomba niwaahidi wastaafu hawa kwamba pale tu tutakapomaliza, Serikali imeshaji-commit kwamba tutalipa malipo yao yote kuanzia Julai 2015.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu yaliyotolewa na Wizara ambayo hayakidhi viwango.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wastaafu zaidi ya idadi iliyotolewa na hasa walimu, hata Jimboni kwangu Buyungu idadi kubwa ya walimu waliostaafu inaweza ikaakisi idadi ya watumishi walistaafu katika nchi hii. Sababu zilizotolewa za wastaafu hao kutolipwa moja kubwa ni kukosa fedha kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambayo Serikali haijataja.
Swali la kwanza, naomba Serikali ikiri ni lini italipa wastaafu wote kwa kupeleka fedha kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ili wasiendelee kuteseka sambamba na kuwarudisha nyumbani kwao mara baada ya kustaafu? (Makofi)
Swali la pili, wapo wastaafu wa aina mbili, wapo wanaolipwa pensheni na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na wapo wanaolipwa pensheni na Hazina. Wale wa Mifuko wa Hifadhi ya Jamii wanapata monthly pension wale wahazina wanalipwa kwa miezi mitatu (quaterly pension) hali hii inawasumbua na kuwatesa wastaafu wetu. Naomba wastaafu wote walipwe monthly pension kama ilivyo kwenye mkataba wa kazi. (Makofi)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naomba uulize swali, naona unaleta ombi.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Swali la pili dogo, ni lini Serikali itaanza kuwalipa wastaafu wote pensheni ya kila mwezi badala ya miezi mitatu? Ahsante!
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kumhakikishia data nilizompatia ni za kweli na za uhakika, kwa hiyo naomba aamini hao ndiyo wastaafu ambao tunajua wamestaafu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili sababu nilizozitaja ndizo zinazosababisha wastaafu hao wachelewe kulipwa siyo upelekaji wa fedha. Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwenye Mifuko hii ili waweze kulipwa wastaafu hawa na hizi sababu nilizozileta ndizo ambazo tunazifahamu kama Serikali na Mifuko yote imeendelea kupokea fedha kutoka Serikalini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, wastaafu wanaolipwa Hazina kulipwa kwa miezi mitatu mitatu. Naomba nilieleze Bunge lako Tukufu kwamba uamuzi wa Serikali kuelekea kulipa miezi mitatu mitatu lilifikiwa baada ya maombi ya wastaafu hawa kuomba walipwe miezi mitatu mitatu. Kama itaonekana sasa wataomba tena walipwe mwezi moja moja, Serikali haioni ugumu wowote kurejea kule tulikotoka.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona, nina swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, wastaafu ambao wanapitia Mfuko PSPF hivi karibuni Serikali iliongeza kiwango, lakini wastaafu hawa wanakuwa hawalipwi kwa wakati na kwa kiwango ambacho Serikali ilitangaza.
Je, ni lini sasa Serikali itaanza kuwalipa wastaafu hawa kwa kiwango sahihi na kwa wakati muafaka?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu tatizo hili lilkuwepo PSPF, lakini kuanzia Disemba 2015 mpaka leo wastaafu hao wamekuwa wakilipwa pesa zao inavyostahili. Kuanzia Disemba hiyo tumeanza kulipa hao wastaafu shilingi 100,000/= kama ambavyo Serikali iliongeza kiwango hiki kupitia Mfuko wa PSPF na arrears zao mpaka kufikia mwisho wa mwezi huu wa nne wote watakuwa wamelipwa zile arrears za kutoka Julai hadi Disemba.
MHE. SABREENA H. SUNGURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
Mheshmiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali imekuwa na tabia tata ya kuchukua fedha kwenye Mashirika ya Umma kama NSSF, LAPF na Mashirika mengine na kutokuzirudisha kwa wakati, ama kuwekeza katika miradi mfu kama mradi wa Machinga Complex na miradi mingine ambayo imekuwa haina tija Serikalini.
Ni lini Serikali itakoma mchezo huu wa kuchukua fedha ambazo zinawaathiri wachangiaji?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali imekuwa ikichukua fedha na hii ikifuata taratibu zote na Mifuko hii kuingia katika Mikataba ili Mifuko hii iweze kuwekeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali itasitisha utaratibu huu, siamini sana kwamba ni sahihi sana Serikali kusitisha, kama Mifuko inaweza kuwekeza na wakaingia katika mikataba ambayo tunaita ni Win Win Situation kati ya Serikali na Mifuko naamini ni sehemu nzuri ya uwekezaji kwa mifuko yetu hii. Kwa hiyo, naomba tuendele kufanya hivyo.
MHE. JAMAL KASSIM ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza:
(a) Kwa vile Naibu Waziri ameeleza kwamba kuna database maalum ambayo TRA wanayo na kule Zanzibar inatumika, je, huu mfumo una tatizo gani, kwa sababu mizigo yote ambayo inapitia Zanzibar kuja Bara asilimia 100 ya mizigo ile inatozwa kodi inapoingia Tanzania Bara, wakati sheria inayotumika ni hiyo moja, na mamlaka ambayo inasimamia kodi na Kamishna ni huyo huyo mmoja?
(b) Mheshimiwa Naibu Waziri, alieleza katika jibu lake kwamba endapo vitu vinatoka Zanzibar kuja Bara wanaagalia tozo la awali ambalo lilitozwa Zanzibar na kuangalia ile tofauti ambayo kwa mujibu wa database zao wanam-charge yule mtu. Sasa je, kwa mtu ambaye ana tv moja anapopita bandarini pale kutokea Zanzibar hana entry…
NAIBU SPIKA: Naomba uulize swali Mheshimiwa Jamal,
MHE. JAMAL KASSIM ALI: Ahsante Mheshimiwa NAibu Spika, je, mtu ambaye kwa vitu ambavyo ni item moja moja kama tvna redio anapotoka Zanzibar kuja Bara wanatumia mfumo gani wa kukokotoa hiyo kodi?
NAIBU WAZIRI WA FEHDA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kodi inazotozwa kwa bidhaa zinazotika Zanzibar kuja huku kwetu, kwanza naomba nisahihishe, mfumo huu wa Import Export Commodity Database unaotumika Tanzania Bara kule Zanzibar hautumiki. Ndiyo maana inaonekana kule ambako hawatumii mfumo huu, bidhaa kule tathmini inapofanyika mara nyingi huonekana ipo chini ya thamani ya kiwango ambacho kinatakiwa kulipiwa kodi inapokuja Tanzania Bara.
Hivyo ndiyo maana bidhaa zinazotoka Zanzibar kuja huku zinatozwa tena kodi. Siyo kodi mara mbili lakini ni kuangalia utofauti wa kodi wa thamani, zilizothaminiwa kutoka Zanzibar na ambazo zimethaminiwa huku Tanzania Bara. Hivyo, tunaomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar waweze kufanya haraka kujiunga na mfumo huu, ili kwa pamoja hili tatizo wanalopata wafanyabiashara wetu wasiweze kulipata.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu bidhaa hiyo moja moja, mfumo ni huohuo mmoja, inapofika kama haikuzalishwa Zanzibar, inapofika Forodhani inatakiwa ichajiwe utofauti ule wa kodi ambao utaonekana ilichajiwa Zanzibar na huku Tanzania Bara. Ahsante.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini kilichokuwa hasa kinatakiwa kipatiwe ufafanuzi, pamoja na majibu mazuri, tunafahamu namna ambavyo mapato ya Serikali yanapatikana kutoka Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Sasa tunachouliza hapa, miradi mingi ambayo imekuwa ikianzishwa kutoka kwenye Halmashauri inayotegemea fedha kutoka Serikali Kuu, fedha hizi haziji kwa wakati na badala yake miradi mingi sana inakuwa mwaka unaisha, miradi inakaa miaka mitano haikamiliki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tunataka tu kufahamu, miradi hii mingine ambayo kwa kweli ingekamilika ingekuwa msaada mkubwa sana kwa wananchi; kwa mfano, kwenye Jimbo la Nyamagana, uko mradi wa maji wa Fumagila, una zaidi ya miaka mwili sasa na umebakiza fedha kidogo sana kutoka Serikali Kuu, kiasi cha shilingi milioni 256 hazijapatikana mpaka leo. Ni lini fedha hizi zitapatikana ili maji yanayokadiriwa kusaidia watu zaidi ya 16,000 yaweze kuwasaidia kwa wakati na kupunguza mzigo kwa akina mama? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi ni kwamba upungufu wowote unaotokana katika vyanzo viwili vya kuchangia katika bajeti yetu hupelekea tatizo hilo, lakini Serikali imejipanga na kwa pamoja tumeona kwamba fedha hizi sasa zimeanza kutolewa. Miradi yote ambayo haijakamilika, Serikali imedhamiria kuendelea kupeleka pesa ili miradi hii iweze kukamilika. Pamoja na mradi wake wa maji alioutaja wa Nyamagana uliobakiza shilingi milioni 200, ninamwahidi kwamba Serikali itapeleka fedha hizo ili kukamilisha mradi huo pamoja na miradi mingine yote ambayo imefikia katika hatua nzuri za utekelezaji.
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naomba niulize swali dogo la nyongeza. Miradi mingi ya maendeleo imekuwa haifanyiki, sababu kubwa pia ni kutokana na baadhi ya gharama za uendeshaji na Halmashauri zetu kutokupelekewa fedha, kwa mfano gharama za kusimamia mitihani. Je, Serikali inajipangaje kulipa madeni hayo kabla mwaka huu wa fedha wa 2015/2016 haujaisha?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbogo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi na katika jibu la swali la nyongeza la Mheshimiwa Mabula, Serikali imejipanga vizuri, mapato yanaongezeka na miradi yote itapelekewa pesa ili iweze kukamilika kwa wakati.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri amejibu baadhi ya maeneo ambayo Mkaguzi Mkuu wa Muungano amekuwa akiyafanyia ukaguzi. Kwa nini mpaka sasa Mfuko wa Kuchochea Maendeleo wa Jimbo, haujawahi kufanyiwa ukaguzi na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Jamhuri ya Muungano?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema ukaguzi wa Mfuko wa Jimbo hufanywa na Mkaguzi Mkuu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini kwa pamoja huwa wanashirikiana kufanya ukaguzi huu na Mkaguzi wa Zanzibar, kwa upande wa Zanzibar. Kwa swali lako la kwa nini, nina imani kuwa Mfuko huu utafanyiwa ukaguzi pale muda utakapofika na ukaguzi huo utafanyika.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona. Mkaguzi Mkuu huwa anakagua mashirika mengine, lakini ningependa kujua au kwa niaba ya wengine pia, yeye huwa anakaguliwa na nani?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mkaguzi Mkuu naamini yeye pia hujikagua mwenyewe.
Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango.
MHE. UPENDO F. PENEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Kwa kuwa, ulipaji wa kodi ni suala la kizalendo na kwa kuwa, suala la ulipaji wa kodi ni wajibu wa kila mwananchi ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vile vile kwa kuwa Wabunge, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Majaji, ni wanufaika kutokana na mishahara na faida mbalimbali tunazozipata kutokana na kodi ambazo wananchi wanalipa.
Je, ni lini Serikali sasa italeta marekebisho ya Income Tax inayompa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Rais wa Zanzibar msamaha wa kodi kwenye mishahara yao? Pia ni lini Serikali italeta marekebisho kwenye sheria inayowapa Majaji wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania misamaha ya kodi kwenye mishahara yao ili wote kwa pamoja tutimize wajibu wa kiraia wa kulipa kodi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyokiri yeye mwenyewe kulipa kodi ni haki ya kila mtu na ni wajibu wa kila mtu. Napenda kumhakikishia Mheshimiwa Upendo pamoja na Bunge lako Tukufu kwamba, muda sahihi utakapofika wa kuleta marekebisho ya Sheria hii tutaileta hapa Bungeni na marekebisho yatafanyika na watu wote watalipa kodi kwa msingi sahihi unaotakiwa. Pia naomba nimkumbushe kuwa, siyo kwamba Mheshimiwa Rais halipi kodi! Mheshimiwa Rais analipa kodi. Nashukuru.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi kuuliza swali la nyongeza. Ili misamaha ya kodi iweze kupungua kufikia asilimia moja ni pamoja na kuhakikisha kwamba sheria zilizopitishwa na Bunge hili zinatekelezwa kikamilifu. Kumekuwa na parallel system, mfano TIC kumekuwa na kikao cha TIC na TRA ambapo TIC ikipokea maombi ya wale wanaoitwa
Strategic Investors wanakaa kikao na wanachagua baadhi ya bidhaa wanazipa msamaha wa kodi. Jambo hili litakoma lini kufanyika? Kwa sababu, pia, linawaweka katika mtego wafanyakazi wa Mamlaka ya Mapato ambao wakishiriki kikao hicho ambacho kinatoa msamaha…
Mheshimiwa Naibu Spika, lini Serikali itahakikisha kwamba, Sheria za Kodi zinatekelezwa kama zilivyopitishwa na Bunge? Kusiwe kuna parallel system?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumhakikishia kwamba, sheria hizi zinatekelezwa kama ambavyo zimepitishwa na vikao hivi huwa vinafanywa kwa pamoja kati ya wataalam wetu waliopo kwenye TIC na wale wa Mamlaka ya Mapato Tanzania. Inapofikia sehemu ya discussion kuhusu kodi wataalam hawa hukaa pamoja kuona ni jinsi gani ya kutoa misamaha hii ya kodi. Hakuna sehemu ambako Wataalam wa upande mmoja hukaa peke yao katika kufikia maamuzi haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nalithibitishia Bunge lako sheria zetu kama zinavyopitishwa na Bunge zinatekelezwa kama tulivyopitisha.
MHE. ESTER N. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimemsikiliza Naibu Waziri wa Fedha kwa makini, kwa jinsi alivyojibu ametutajia figure kubwa sana ambazo zimeenda katika sekta ya kilimo, lakini ni wazi na Waheshimiwa Wabunge wanajua bado wakulima wetu kilimo chao ni cha kusuasua na wanalima katika mazingira magumu. Hata wale ambao wanajitokeza katika kilimo cha umwagiliaji wakiwemo watu wangu wa Tamau, Nyatwali na maeneo mengine wanakosa vifaa. Mna mkakati gani wa kuhakikisha hizi figure zinaendana na hali halisi ya mkulima mmoja mmoja?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nimshukuru kwa kuelewa kwamba kiasi hiki nilichokitaja ndicho ambacho kimetoka Benki ya TIB (Tanzania Investment Bank) kwenda katika miradi ya kilimo na miradi mingine niliyoitaja. Mimi kama Naibu Waziri wa Fedha na Mipango jukumu langu ni kuhakikisha pesa hizi zinafika kwa wale wanaomba pesa hizi. Kwa hiyo, naamini tutafanya kazi kwa ushirikiano mzuri mimi na Waziri wa Kilimo, mtani wangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ili tuhakikishe sasa pesa hizi zinawanufaisha walengwa na zinaweza kukidhi mahitaji yale waliyoomba.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni takribani miaka 13 toka Wilaya hii ya Kilindi imeanzishwa. Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana na mimi kwamba, pana umbali mkubwa sana kati ya Wilaya ya Handeni iliko ofisi ya Mamlaka ya Mapato na Kata mbalimbali za Jimbo la Kilindi hususani katika Kata ya Pagwi. Je, ni lini sasa utafiti huu utakamilika ili wananchi wa Kilindi waweze kunufaika na huduma hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa ametaka kujua ni lini utafiti huu utakamilika. Kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba pamoja na utafiti huu kukamilika pia tunaangalia potentials ya ukusanyaji yaani cost and benefit analysis ya kuanzisha ofisi hizi kila Wilaya. Kwa sasa hivi nguvu nyingi tunazielekeza katika kuanzisha ofisi za Mamlaka za Mapato katika mikoa mipya ambayo imeanzishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo naendelea kusema kwamba namwomba Mheshimiwa Kigua aendelee kuongea na wananchi waendelee kulipa kodi kupitia Wilaya yao ya mwanzo kabla ya Kilindi kuanzishwa. Pia tutakapokamilisha utafiti huu na tukaona kwamba kuna potential kubwa ya kupata mapato ya kutosha Wilaya ya Kilindi, basi hatutasita kuanzisha ofisi hii katika Wilaya ya Kilindi na wilaya nyingine zote za Tanzania ambazo hazina Ofisi.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa benki nyingi hapa Tanzania zinatoa mikopo kwa riba kubwa sana na zinafanya wafanyabiashara ama wananchi wa Tanzania kukopa lakini kutokurudisha mikopo hiyo kwa wakati kutokana na riba kubwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha benki hizo zinapunguza riba hizo?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa hivi sasa kumejitokeza taasisi nyingi ambazo zinatoa mikopo, lakini hazifuati taratibu za kitaalamu je, Serikali inalijua hilo na kama inalijua hilo inazichukulia hatua gani taasisi kama hizo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kumpongeza Mheshimiwa Faida Bakar kwa umakini wake wa kufuatilia masuala ya kifedha hapa nchini. Hili ni swali lake la pili katika Bunge hili nalijibu akiulizia masuala haya, hongera sana Mheshimiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kumekuwa na riba kubwa, lakini naomba tufahamu kuwa kufuatia mabadiliko ya mfumo wa kifedha hapa nchini kuanzia mwaka 1991, Serikali ilijitoa katika uendeshaji wa moja kwa moja wa shughuli za kifedha hapa nchini, ili kuruhusu ushindani huru na kuboresha huduma katika sekta yetu ya fedha. Hivyo, viwango vya riba na mikopo zinazotozwa na benki zetu na taasisi nyingine za kifedha zinapangwa kutokana na nguvu ya soko huria ambalo tuliamua wenyewe kuingia katika soko hilo.
Mheshimiwa Spika, pia napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kwamba katika upangaji wa viwango hivyo vya tozo mbalimbali na riba benki pia na taasisi zetu za kifedha huzingatia gharama za upatikanaji wa fedha, pia gharama za uendeshaji na sifa alizonazo mkopaji katika kuliendea hilo. Hivyo Serikali pia tunaendelea kuwasisitiza mabenki yetu pamoja na taasisi zetu za kifedha kutumia takwimu za credit reference bureau ili kuweza kujua taarifa halisi na historia za wakopaji na pia ushindani uliopo ili tuweze kushusha riba hizi, lakini kama Serikali hatuwezi kuingilia tena katika soko hili.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili Mheshimiwa Faida Bakar, amependa kujua kwamba kumekuwepo na taasisi nyingi za kifedha na je, zile ambazo hazifuati utaratibu je, Serikali ina mpango gani wa kuzitambua na kuzirasimisha?
Napenda kumjibu Mheshimiwa Faida Bakar kwamba Serikali inafahamu tatizo hili la Taasisi zilizopo za binafsi ambazo zipo na zinasumbua sana wananchi wetu. Katika kulitambua hilo Serikali kwa sasa iko katika mpango wa kuandaa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya mwaka 2016 ambapo sasa hivi ipo katika hatua nzuri, itapelekwa kwenye Baraza la Mawaziri na hatimaye tutaweza kuwa na Microfinance Act itakayoweza kudili na tatizo hili moja kwa moja. Nashukuru.
MHE. RAISA ABDALLAH MUSA: Mheshimiwa Spika, napenda nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri swali dogo la nyongeza. Kutokana na mfumo wa mabenki mengi, utitiri wa mabenki mengi hapa nchini, Serikali imejipanga vipi kuyasimamia mabenki yale na kuyawezesha ili iweze kuwakopesha wateja na kuleta tija kwa Taifa letu?
Mheshimiwa Spika, nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwamba Serikali kupitia mabadiliko ya mfumo uliotokea mwaka 1991 ilijitoa katika kuendesha moja kwa moja sheria za kifedha hapa nchini, lakini hayajaachwa huru, Benki Kuu inayasimamia na ndiyo maana nimesema hata hizi taasisi ndogo ndogo tunaandaa Sera ya Taifa ya hizi taasisi ndogo ndogo za fedha ili zote tuweze kuzisimamia kiuhakika, lakini siyo kuingilia katika uendeshaji wa huduima hizi. Nina imani kubwa taasisi zetu hizi za kifedha zinafanya kazi kwa ajili ya Watanzania na kwa ujumla zinatenda vizuri ndiyo maana watu wengi wanaweza kuzifikia na kupata mikopo pale wanapohitaji.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kumuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Waziri, nataka kujua ni lini Serikali itasambaza mashine za EFD katika Mikoa yote ya Tanzania, ili mwananchi aweze kulipa kodi kihalali na kuweza kulipatia Taifa mapato? (Makofi)
Swali la pili; kuna changamoto katika mtandao, changamoto hii ya mtandao inapelekea kukatika kwa mawasiliano kati ya mashine hizi na TRA. Mfano mnunuzi yupo kituo cha mafuta X akiwa safarini kuelekea Mkoa Y na ikatokea kuna changamoto hiyo, je, mnunuzi anatakiwa afanyeje ikiwa juzi tu tumepitisha sheria kwamba lazima mtu achukue risiti?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nilithibitishie Bunge lako Tukufu kwamba nia ya Serikali yetu ni kusambaza mashine hizi nchi nzima. Kama tunavyofahamu jambo lolote lina gharama na mashine hizi pia zina gharama, kwa sasa Serikali imeanza kugawa mashine hizi za EFD katika Mkoa wa Dar es salaam kwa wafanyabiashara wadogo wenye mauzo ghafi kati ya shilingi milioni 14 hadi milioni 20. Katika awamu ya kwanza Wizara yangu imepanga kugawa mashine za EFD 5,703 na mpaka leo tayari wafanyabiashara 118 wameshachukua mashine zao. Naomba pia niwashajihishe wafanyabiashara wote wa Dar es salaam ambao waliainishwa kuchukua mashine hizi sasa waende wakachukue mashine, kama ambavyo tumesikia kwenye vyombo mbalimbali vya habari kwamba mashine hizi zipo lakini wafanyabiashara hawataki kujitokeza kwenda kuchukua mashine hizi. Nawaomba wafanyabiashara wafike na wachukue mashine hizi katika Mamlaka yetu ya Mapato. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la Mheshimiwa Neema ameuliza changamoto katika mtandao. Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kwamba Serikali yetu pia imefanya jitihada ya kusambaza mkongo wa Taifa nchi nzima. Kwa hiyo, changamoto hii ya mtandao naamini haina muda mrefu itafika mwisho na pia naomba niseme na niwaombe wafanyabiashara, wamekuwa wakisingizia changamoto ya mtandao kumbe hakuna tatizo la mtandao. Naomba niwaambie ni vizuri wakaweza kutumia sasa fursa hii ya kuenezwa kwa mkongo wa Taifa na kuweza kutumia mashine hizi katika kutoa risiti pale ambapo wanauza au wanatoa huduma yoyote kwa wananchi. Nimekuwa nikiongea na wafanyabiashara nikiwauliza swali na Waheshimiwa Wabunge naamini ninyi ni mashahidi nani amewahi kufika katika mabenki ya biashara akaambiwa mtandao upo chini, hakuna. Kwa hiyo, hii pia ni danganya toto ya wafanyabiashara, naomba niwaambie sasa Serikali tumeingia vizuri na tunaanza kazi kila mmoja aweze kutoa risiti hizi za mashine ya EFD.
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ni kupata taarifa za wafanyabiashara ili waweze kulinganisha na maandalizi ya kumbukumbu zao za hesabu. Sasa katika uhasibu kuna marekebisho ya kiuhasibu, inatokea mtu anatoa kitu kinaitwa credit note au debit note ili kufanya masahihisho. Lakini kwa sasa mfumo huu wa electronic signature device hauchukui marekebisho ya kiuhasibu. Je, ili kuondoa hali ya sintofahamu na kulinganisha kumbukumbu za TRA na wafanyabiashara, Serikali ipo tayari kubadilisha mfumo wake na kuingiza hizi credit note au debit note katika marekebisho ya kiuhasibu ili ziweze kusomeka katika mtambo wa TRA na kurahisisha kazi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi; lengo la mashine hizi ilikuwa ni kupata taarifa na kumbukumbu sahihi za wafanyabiashara na mauzo yao, lakini kama kuna jambo lolote ambalo litaweza kuboreshwa zaidi Serikali yetu iko wazi kabisa, naomba tushirikiane ili tuweze kuhakikisha kumbukumbu zote zinaingia katika mfumo huo. Kwa sasa, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba tumeanza na hizo kumbukumbu za mauzo na mapato ya wafanyabiashara ila haya mengine yote pia tunaendelea kuboresha mfumo wetu, nina imani kubwa yote yataingizwa kwenye mfumo huu.
MHE. ZAYNABU M. VULU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza ni kutaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia akina mama walioanzisha VICOBA kwa kuongezewa mtaji wao? Pia Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha taasisi binafsi zinazotoa mikopo kuacha kunyanyasa akina mama wanapochelewa kulipa mikopo yao kwa kuwanyang‟anya vifaa vyao vya matumizi na vinavyowaendeshea maisha? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni lini Serikali itashawishi mabenki kutupelekea benki kwenye Wilaya ya Mafia na Jimbo la Utete? Kwa sababu Makao Makuu ya Wilaya ya Rufiji ni Utete lakini mpaka leo hapo Utete hakuna huduma inabidi waende Kibiti kufuata huduma. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili japo yameonekana kama manne ya Mheshimiwa Zaynabu Vulu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ni akina mama kuongezwa mtaji kwa kuwa wameanzisha VICOBA. Kwanza kabisa naomba niwapongeze akina mama wote nchini kwa kuonesha ujasiri wao katika kuungana katika vikundi na kuanzisha VICOBA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba Serikali imeweka mazingira mazuri na tayari taasisi za kifedha au benki za jamii zinaanzishwa hivyo nawashauri akina mama hawa na mimi nitashirikiana nao kama mama kuhakikisha kwamba tunaanzisha taasisi au benki yetu ya kijamii ya wanawake sehemu yoyote ile. Naomba nitoe nafasi hiyo, tushirikiane kwa pamoja Wabunge wanawake ili tuweze kuungana na akina mama hawa kuanzisha benki ya wanawake ya kijamii sehemu yoyote ile ndani ya nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ya swali hili la kwanza ilikuwa ni taasisi za kifedha zinazokopesha ziache kuwanyanyasa akina mama. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba kama nilivyojibu wiki moja iliyopita Serikali inaanzisha rasimu ya sera kwa ajili ya taasisi hizi ndogo za fedha ili sasa kuweza kuzikagua na kuziwekea sheria na taratibu ya kuweza kufanya kazi na kuacha kuwanyanyasa akina mama. Sera hii itakapokuwa tayari, nina uhakika kabisa taasisi hizi zitaacha kuwanyanyasa akina mama. Pia naomba niwashajihishe taasisi zote hizi zinazotoa mikopo kwa akina mama ziache utaratibu huu wa kuwanyanyasa akina mama. Tufuate taratibu zote za utoaji wa mikopo kama vile kuangalia uwezo wa mlipaji anayekopa kabla hujamkopesha kuliko kumkopesha tu kwa kuonekana wako kwenye kikundi halafu baadaye unakuja kuwanyanyasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, nilisema ameuliza maswali mawili lakini yanaonekana kama manne, kwa hiyo, kulikuwa na sub-questions. Napenda kulijibu swali hili, kwamba ni lini Serikali itaweza kuzishawishi benki kupeleka matawi yao Mafia na Rufiji?
Namuomba Mheshimiwa Zaynabu Vulu tushirikiane tuone ni jinsi gani ya kuongea na benki zetu na hasa benki yetu ya NMB na CRDB, nina uhakika wakienda ku-access mazingira ya Mafia wataenda kufungua tawi lao sehemu hii. Naomba tukae na Mheshimiwa Zaynabu Vulu tuone ni jinsi gani ya kushughulikia suala hili.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kunipa niulize swali la nyongeza. Wafanyakazi wamekuwa wakikatwa fedha zao na kupelekwa kwenye huu mfuko wa PSPF. Lakini wafanyakazi hawa wanapokuwa wamemaliza huo muda wanacheleweshewa kupewa mafao yao. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuona kwamba, wafanyakazi hawa wanapomaliza muda wao wawe wanaandaliwa cheque zao mapema ili kusudi ziweze kuwasaidia katika kufanya shughuli zao wanazokuwa wamejipangia kuliko hivi sasa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, je, Mheshimiwa Waziri amejibu amesema wameshaanza kulipa; anaweza sasa akanisaidia mimi orodha ya Mkoa wa Tanga, hususan Korogwe, wale ambao wamekwishalipwa ili wasiendelee kunieleza kwamba wanadai? Nipate ile orodha ili iweze kunisaidia.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa swali lake la kwanza alilouliza kuhusu kucheleweshewa malipo, kama ambavyo Serikali imekuwa ikitoa majibu humu Bungeni ni kwamba kucheleweshewa huku hakutokani na Serikali, kunatokana na waajiri ambao wanachelewesha kufikisha nyaraka za wastaafu hawa katika Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii. Hivyo, nitoe tu wito wangu kwa waajiri wote wajitahidi kupeleka nyaraka zote zinazostahili kwa wastaafu miezi mitatu au sita kabla mstaafu hajastaafu ili tuweze kulipa mapema iwezekanavyo. Wakiweza kufanya hivyo, Waheshimiwa Wabunge tunaweza kabisa mstaafu anapokuwa amestaafu nyaraka zake zimekamilika na cheque yake itaweza kulipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, Mheshimiwa Mbunge naomba nifanye kazi mimi na wewe kuhusu wastaafu wote wa Wilaya ya Korogwe wanaolipwa na Mfuko wetu wa PSPF, tunapomaliza Kikao hiki cha Bunge naomba tushirikiane ili upate orodha halisi ya waliostaafu na orodha halisi ya waliolipwa katika kipindi hiki. (Makofi)
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Naomba kuuliza swali la nyongeza, Serikali ina mkakati gani sasa kwa watumishi ambao wamestaafu kwa hiyari ama wengine wamebadilisha kazi kwa mfano kuwa Wabunge, ili kuendelea kuchangia Mfuko huu wa PSPF badala ya kuwaondoa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati uliopo kati ya Serikali na watumishi hawa, nadhani ni ndani ya mtumishi yeye mwenyewe kwamba kama anaona anaweza kuendelea kulipa anaweza kuongea na watumishi wa mfuko huu, Wakurugenzi wetu wote na wote wako tayari na wanapenda kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mussa Sima nikwambie mimi ni mmoja wa waliokuwa watumishi wa Serikali na sasa naendelea kuchangia malipo yangu baada ya mimi kwenda kuongea na Mkurugenzi wa Mfuko wa PSPF na sasa mimi naendelea kuchangia.
Kwa hiyo, nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge wote, Waheshimiwa Watumishi wote na Watanzania kwa ujumla wanaoona wanaweza kuendelea kulipa basi waende wafike kwenye mifuko hii na wataweza kuendelea kulipa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WATU WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza kabisa niwapongeze Waheshimiwa Naibu Mawaziri wote wawili kwa majibu mazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama tu kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba sheria hizi za malipo ya pensheni na mifumo ya kuchangia katika mifuko ya pensheni zimehuishwa na sasa kila mtumishi wa umma ama mtumishi katika sekta binafsi anapohama kiajira kutoka ajira moja kwenda ajira nyingine ama anapotaka kuhamisha mafao kutoka mfuko mmoja kwenda katika mfuko mwingine kwa mujibu wa sheria sasahivi anaruhusiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni suala tu kila mtu kufikiria na kuona ni namna gani anataka kuendelea kuhuisha mafao yake na anaweza kuhusiaha katika mfuko wowote kwa kuhamisha kutoka mfuko mwingine kwenda mwingine kama anabadilisha ajira ama anaamua kufanya hivyo na sheria sasa hivi zinaturuhusu. (Makofi)
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu kwa pensioners ambao hawalipwi kupitia Hazina moja kwa moja kwamba, vile viwango vipya vya malipo hawajaanza kulipwa mpaka hii leo. Na haya malalmiko yamekuwa ni ya muda mrefu sana. Naomba commitment ya Serikali ni lini wastaafu hawa wataanza kulipwa viwango vyao vipya pamoja na arrears zao?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimekuwa nikiliarifu Bunge lako Tukufu ni kwamba watumishi wote ambao wanalipwa kupitia Hazina walianza kulipwa fedha zao za nyongeza tangu mwaka jana mwezi wa saba, 2015. Kwa mifuko ambayo haijaanza kulipa kama ambavyo nilisema mwanzo, nyongeza hizi, sasa hivi Bodi za Mifuko hii zinamalizia kufanya maamuzi, ili waweze kuanza kulipa nyongeza ambayo ni ya 50,000 kama ilivyotangazwa na Serikali.
MHE. WILFRED M. LWAKATARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kuniruhusu kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa Mkoa wa Kagera enzi hizo ukiitwa Ziwa Magharibi baada ya kupata uhuru ilikuwa ni miongoni mwa mikoa minne ambayo ilikuwa na utajiri na pato kubwa ikiwa ni Kilimanjaro, Dar es Salaam pamoja na Mbeya, na wakati huo ikiwa na Chama cha Ushirika (BCU) ambacho kilikuwa na nguvu kubwa kiasi cha kuikopesha hata Serikali, sasa maswali yangu.
La kwanza, je, Serikali itakubaliana na mimi kwamba miongoni mwa mambo ambayo yamesababisha umaskini kwanza ni vita ya Kagera ambayo hata baada ya kualizika na Serikali ya Uganda kulipa fidia, wananchi hawakupewa fidia yoyote?
Pili, ugonjwa wa UKIMWI, lakini tatu Chama cha Ushirika cha KCU ambacho kimesambaratika na hususan kutokana na mambo mengi ya kisiasa badala ya kutetea zao la kahawa. Lakini pia Reli ya Kati ambayo kimsingi imesambaratika na haifiki Kemondo na hivyo wananchi wa Mkoa wa Kagera kupokea bidhaa kwa njia ya barabara ambayo inawagharimu vibaya sana.
Je, Serikali haioni kwamba kuna haja pamoja na mambo aliyozungumza ambayo kimsingi bado yanaeleaelea na hayana mashiko, kuweka mkakati mahsusi wa kuyaweka katika utekelezaji na hata kuyaweka katika mpango wa BRN (Matokeo Makubwa Sasa), lakini sambamba na hilo kwa kupitia Mpango wa TASAF, kama Serikali imetathmini kwamba mkoa ni maskini na kaya ni maskini kwamba bajeti ya TASAF iongezeke ili kaya ziweze kupokea pato zaidi na kaya ziweze kuongezeka?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kufuatana na sababu zilizotolewa na takwimu zilizotolewa, je, hizi takwimu zinatoa takwimu sahihi ambayo inaashiria ni kwa Wilaya zote au ni kwa baadhi ya wilaya zilizopo ndani ya Mkoa wa Kagera ndiyo zenye umaskini wa namna hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nakubaliana na sababu alizozisema na ndiyo maana Serikali iko kwenye mpango mkakati wa utekelezaji wa mpango wetu ambao tumeuwasilisha humu Bungeni kama alivyosema tuje na mpango mahsusi wa utekelezaji kupeleka kwenye BRN, Serikali iko kwenye mchakato wa kuja na utekelezaji wa maazimio yote na malengo yote yaliyopo ndani ya BRN.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo utakumbuka ni kwamba tayari sasa hivi mchakato wa kutengeneza Reli ya Kati kwa standard gauge unaanza mwezi Disemba tunaanza utekelezaji na ambayo inaelekea upande huohuo wa Mikoa ya Magharibi na Kagera ikiwepo ili tuweze kufungua uchumi wa Mkoa wa Kagera na uchumi wa mikoa mingine ya upande wa kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu takwimu hizi, naomba niliambie Bunge lako Tukufu, takwimu hizi ni sahihi na zinaashiria Mkoa mzima wa Kagera kwamba upo katika kiwango cha umaskini wa asilimia 39 kama nilivyosema.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naomba niulize swali la nyongeza.
Kwa kuwa matatizo yaliyopo kwenye Mkoa wa Kagera, Mkoa wa Mwanza pia ni moja kati ya mikoa iliyotajwa kuwa mikoa maskini, sasa ningependa kujua mikakati ya Serikali mbali ya majibu mazuri na mipango ya miaka mitano na mwaka mmoja, ina mkakati gani wa kuwawezesha wafanyabiashara wadogo na wa kati ili kuwa sehemu ya kuhakikisha na wao wanakuwemo kwenye mpango wa kuhakikisha umaskini huu unatoweka wakiwa wana nafasi nzuri ya kufanya biashara zao kwa uhuru?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema na kama tulivyoainisha kwenye mpango wetu wa mwaka mmoja na mpango wa miaka mitano kwamba sasa hivi tunaangalia jinsi ya kuanzisha na kuendeleza viwanda vidogo vidogo pamoja na viwanda vikubwa vikubwa, vya kati pia ili tuweze sasa kutengeneza ajira kwa watu wetu. Na hii ni pamoja na kuwawezesha wafanyabiashara hao wadogo na wa kati ili waweze kupata bidhaa zao kwa bei nafuu na pia tuangalie pia wafanyabiashara ambao wako katika sekta ya kilimo kwa sababu tumesema viwanda vidogo, viwanda vya kati na vikubwa vitatumia malighafi zinazozalishwa hapa nchini kwa hiyo ni mpango wa Serikali yetu kuweza kuwawezesha watu hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa sababu tunakuja na Microfinance Act mwezi huu au mwezi wa 11 ni uhakika kwamba watu hawa, wafanyabiashara wadogo na wa kati watapewa elimu ya ujasiriamali na jinsi gani ya kuendeleza biashara zao pamoja na kuwezeshwa mitaji ni moja ya mikakati ya Serikali yetu.
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa mujibu wa takwimu ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri ametupatia, Deni la Taifa sasa mpaka Juni mwaka huu limefikia shilingi trilioni 51 na bilioni 40. Kiwango hiki cha fedha ni almost mara mbili ya bajeti ya Taifa. Wakati huo huo ukigawanya deni hili kwa Watanzania milioni 45 kila Mtanzania leo atakuwa anadaiwa shilingi 1,134,222.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kukopa ni muhimu katika wakati mwingine ili kuweza kusukuma mbele shughuli za kimaendeleo, lakini ulazima wa kukopa kwa kiwango ambacho tunaweza kukilipa kwa wakati ili Taifa liondokane na mzigo wa riba pamoja na kulimbikiza madeni liweze kujielekeza mapato yake zaidi katika kushughulikia mipango ya maendeleo, ni vyema tuwe na kiwango cha ku-control ukopaji wa Serikali.
Sasa swali langu la mwisho ni hili, tutakumbuka wakati wa Awamu ya Tatu, wakati wa Mheshimiwa Mkapa, Tanzania ilikuwa mojawapo ya nchi zilizokuwa zimepata sifa ya kuwa miongoni mwa nchi zilizosamehewa madeni kupitia mpango wa HIPC (Heavily Indebted Poor Countries) ambapo Deni la Taifa liliweza kusamehewa na likashuka chini ya dola bilioni 10 na almost tulikuwa tunamaliza Deni la Taifa.
Je, ni kwa nini Serikali sasa hivi, kwa sababu bado mpango wa HIPC upo chini ya World Bank na IMF, ni kwa sababu gani Serikali isione uwezekano tena wa kufanya initiative ya kurudishwa katika Mpango HIPC ambao unasimamiwa na World Bank na IMF ili tupunguze mzigo huu wa madeni na hizo pesa tuzielekeze zaidi kwenye shughuli za kimaendeleo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haijaondoka kwenye mpango huo wa kusamehewa madeni na bado tunaendelea na mchakato huu kwa kushirikiana na IMF pamoja na World Bank. Zipo nchi ambazo zilikuwa katika mpango wa kuhakikisha tunasamehewa madeni kama nchi yetu lakini zilisitisha kutokana na migogoro ambayo ipo ndani ya nchi hizo, moja ya nchi hizo ilikuwa ni Iraq, Iran pamoja na nchi nyingine zenye migogoro ambazo zilisitisha sasa kusamehewa madeni. Hivyo bado tunaendelea na mchakato huo kuendelea kuwashawishi wadau hao wa maendeleo ili waweze kutusamehe madeni haya.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa ya kitaalam, lakini nilitaka kuongezea nyongeza tu na kuwatoa hofu Watanzania kwenye kile alichosema Mheshimiwa Mbowe kwamba ukiligawa deni hilo kwa kila Mtanzania.
Kwanza hakuna siku Watanzania watagongewa mlango wakigawanywa Deni hilo la Taifa na wala katika Taifa lolote hakuna utaratibu wa kupima deni kwa kuangalia mgawanyo wa ujazo wa watu bali Deni la Taifa linapimwa kufuatana na uwezo wa nchi kimapato inavyokusanya na inavyoweza ku-service deni hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo tunapoangalia kukua kwa deni tutakiwa pia tuangalie miundombinu ya nchi yetu imekuwa kwa kiwango gani kwa sababu wazo hilo linafuatana na uamuzi wa nchi inayochukua kwenye miundombinu, hata hivi sasa Waheshimiwa Wabunge tunavyoongelea standard gauge ya reli, tunavyoongelea miradi mikubwa mikubwa kama ya bandari tutakuwa tunaongelea uwezo wa nchi yetu kuweza kuendesha miradi, lakini ujenzi wake utategemea njia hizo hizo za kuweza kukopa. Ndiyo maana hata mataifa makubwa ambayo yameendelea leo hii yana madeni makubwa lakini yana uwezo wa kulipa madeni hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimoja tu ambacho natakiwa nimhakikishie Mheshimiwa Mbowe ambacho Serikali inakifanya, haikopi kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Serikali inapokopa kwa mara zote inakopa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ambayo itazalisha kulipa deni hilo. (Makofi)
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri nina maswali madogo tu ya nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri. Kwanza, je, wanatumia vigezo gani vya usajili wa hivyo VICOBA?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wakiwa wanakopesha wanaanzia na kiwango gani cha hiyo mikopo, ili wananchi nao waweze kukopa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza vigezo vinavyotumika ni kuangalia kikundi husika kinajishughulisha na nini na kama kina wadau muhimu katika kikundi hicho, pamoja na aina ya shughuli kinachotaka kujishughulisha kikundi hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na swali lake la pili, ameuliza ni shilingi ngapi wanakopeshwa, hapa kinaangaliwa tu kikundi husika kina mtaji kiasi gani na kimeomba kiasi gani na hivyo, kuangalia kama wanaweza kukopesheka, kuangalia viashiria hatarishi ndani ya kikundi kile kama waliwahi kukopa na uwezo wao wa ku-manage biashara walianza lini. Kwa hiyo, tunaangalia mtaji wao endelevu na sustainability yao katika biashara wanayofanya.
MHE. AJALI R. AKBAR: Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru Wizara ya Fedha kwa kufanya mipango mizuri na niishukuru sana kutangaza Kariakoo kuwa Mkoa wa TRA.
Mheshimiwa Waziri, leo tumesoma kwenye magazeti yanasema kwamba, kuna mdororo wa uchumi, mpaka kufikia mahali ambapo mabenki hayakopeshi tena wananchi na wameanza kuuza bond zao. Ni nini Wizara ya Fedha inazungumza kuhusu haya mabenki kutokuwakopesha wawekezaji au waanzishaji biashara mpya ili waendelee kuuimarisha huu uchumi?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wizara ya Fedha itoe msimamo wake. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ajali, swali la msingi linahusu VICOBA, sasa maelezo ya jumla kuhusu uchumi, hayo yatamtaka Waziri alete hoja hapa. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge tutaendelea.
MHE. MATTAR ALI SALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kero hii inalalamikiwa sana na wafanyabiashara wetu na hufikia hatua kupoteza wafanyabiashara hawa kuendelea na biashara. Je, ni lini Wizara hii itaanza utatuaji wa kero hii kwa wafanyabiashara wote?
Swali la pili, Wizara itamaliza lini kero hii ya kutatua suala hili la kodi ya wafanyabiashara wanaotoka Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, utofauti huu unatokana na tatizo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutokutumia mfumo nilioutaja kwenye jibu langu la swali la msingi. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea kuishawishi Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kujiunga na mifumo inayotumika ndani ya Idara ya Forodha ili kuondoa changamoto hii inayowakumba wafanyabiashara wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niliambie Bunge lako Tukufu kwamba, progress ni nzuri na kwa kuanzia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika bajeti yake ya mwaka 2016/2017 imeridhia kutumia mfumo wa Import Export Commodity Database kwa bidhaa ya magari yatakayoingia Zanzibar ili kuweza kuondoa changamoto hii. Kwa hiyo, naona huu ni mwanzo mzuri. Tunaendelea kuishawishi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iweze kujiunga moja kwa moja kwa bidhaa zote zinazoingizwa Zanzibar na hatimaye kuletwa Tanzania Bara.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina Mjimbo matatu na Ofisi ya TRA ni moja tu kwa Majimbo yote matatu; je, ni lini Serikali itaipandisha hadhi Ofisi ya TRA, Lushoto na kutoa TIN Number, Motor Vehicle na License za udereva ili wananchi wasipate taabu ya kwenda mpaka Tanga Mjini?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tunajua Wilaya ya Lushoto ina Majimbo matatu na tuna Ofisi moja ya TRA.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mheshimiwa Mbunge atakumbuka ndani ya wiki mbili zilizopita, nilijibu kuhusu ufunguzi wa Ofisi za TRA, lakini kwa kuwa tuna Ofisi ya TRA Lushoto, kinachohitajika ni kupandishwa hadhi; namuomba Mheshimiwa Mbunge tuonane ili tuweze kukaa pamoja na tuone ni jinsi gani sasa tutaweza kuipandisha hadhi ofisi hii ili huduma hizi muhimu ziweze kupatikana kwa ajili ya wafanyabiashara wetu.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini bado nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, kwa kuwa iliyokuwa NBC, Benki iliyokuwa inamilikiwa na Serikali ilikuwa na tawi pale mlalo na ilikuwa inahudumia wakazi wa Mlalo, Mbaramo, Mtae mpaka Mlola; je, kwa nini NMB iliyochukua nafasi ya NBC isitekeleze wajibu huo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa, Mheshimiwa Waziri amesema sehemu ambazo zina mzunguko mkubwa wanaweza wakaongeza ushawishi wa kutengeneza Community Bank; na Jimbo la Mlalo lina mzunguko mkubwa wa fedha; je, ni lini kwa kushirikiana na SACCOS ya Kumekucha Mwamko SACCOS Ltd. wanaweza wakawajengea uwezo ili tuweze kuanzisha hiyo Community Bank? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi ni kwamba Serikali ilijitoa moja kwa moja kuendesha shughuli hizi, lakini Serikali kupitia Wizara yangu itaendelea kuhimiza mabenki kuendelea kusambaza huduma zao kwa wananchi wa vijijini likiwepo na Jimbo la Mlalo. Pia nitalifikisha ombi hili katika Benki yetu ya NMB na kuwashauri kuhusu ombi hili la Mheshimiwa Rashid Shangazi ili tuone sasa NMB inaweza kurejesha huduma ambayo mwanzo ilikuwa ikiendeshwa na Benki yetu ya NBC. Kwa hiyo, nitakaa nao, nitaongea nao na namwomba Mheshimiwa Mbunge tushirikiane naye ili tuweze kuongea na Menejimenti ya NMB ili kurejesha huduma hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili, napenda kumthibitishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania ipo tayari kabisa kutoa ushauri wa kitaalamu na namna ya kuanzisha benki za kijamii. Ninafahamu pale Mlalo hasa maeneo ya Lukozi, maeneo ya Rangwi, Mlalo yenyewe, Shume na Mlola kuna huduma nyingi za kiuchumi, hivyo niko tayari kabisa kuishauri Benki Kuu kwamba sasa tukatoe huduma hizi za kitaalamu kwa wajasiriamali wetu hawa ili waweze kuanzisha Benki ya Kijamii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, kuna society nzuri pale ambayo tukishirikiana nao na mtaji unaotakiwa kuanzisha Community Bank ni shilingi bilioni mbili tu, kwa taarifa nilizonazo, taasisi hii iliyopo pale ina zaidi ya shilingi bilioni moja sasa. Kwa hiyo, wamebakiza sehemu ndogo tu waweze kuanzisha Community Bank. Mheshimiwa Rashid Shangazi tushirikiane ili tuweze kuanzisha Community Bank pale Mlalo.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, niliomba niulize swali lingine la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile huduma hizi za kibenki ni suala la kisera; na kwa vile ni haki ya kila Mtanzania kupata huduma hizi; na kwa vile imebainika kwamba mabenki yetu ya kibiashara hayawezi kufika yale maeneo ambayo hayana tija sana kibiashara; ni lini sasa Serikali itahakikisha kwamba Benki ya Kilimo inayafikia maeneo hayo ambayo hayana tija kwa wafanyabiashara wa kibenki likiwemo Jimbo la Madaba na Jimbo la Mlalo kama ilivyoulizwa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mhagama kama ulivyosikia wakati tunaweka Mezani bajeti yetu ya Wizara ya Fedha, moja katika benki ambazo tunategemea kwamba zitafungua matawi yake zaidi, ni hiyo Benki yetu ya Kilimo. Kwa hiyo, tunaendelea kuijengea uwezo na muda siyo mrefu Benki hii itafungua matawi yake katika maeneo yenye wakulima wetu ili waweze kufaidika na huduma za Benki yetu ya Kilimo.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwa kuwa kuna mtazamo kwamba kila kundi kufungua benki ndiyo jibu la huduma ya benki, siyo jema; na kwa kuwa hapa tulipofikia, huko nyuma tulikuwa na Benki ya Posta ambayo iko kila mahali na watumiaji wa benki ni hao hao wananchi wa eneo lile; je, ni kwa nini sasa Serikali isiipe uzito Benki ya Posta ikasambaa kote?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, katika benki ambazo zinakuja juu sasa ni Benki yetu ya Posta. Tumeiwezesha vizuri, Menejimenti yake imekaa vizuri sasa, imezindua huduma nyingi ambazo hata benki nyingine kubwa za kibiashara zimeshindwa kuanzisha huduma hizo. Kwa hiyo, ni imani yangu kubwa Benki ya Posta ndani ya muda mfupi ujao itarejesha hadhi yake ndani ya nchi yetu ya Tanzania.
Nawaomba Waheshimiwa Wabunge, tuendelee kuiunga mkono Benki yetu ya Posta, tufungue akaunti kule, tuiwezeshe sisi kama shareholders muhimu ili Benki ya Posta iweze sasa kurejea. Tuko vizuri na inakimbia Mheshimiwa Shally, itafungua matawi yake sehemu zote nchini.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nina maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, Serikali ya Awamu ya Tano katika matendo yake imeonekana inasimamia haki. Nataka kujua kama pato la kodi hii Serikalini kwa magari yaliyosimama kwa muda mrefu kwa sababu za msingi, lina tofauti yoyote na pato analolipata mwananchi au mtumishi hewa kutoka Serikalini?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ni ushauri. Kwa kuwa magari yanayotozwa kodi hii hutumia mafuta na kwa kuwa kodi hii imekuwa na adha katika ukusanyaji wake na ni kero pia kwa wananchi: Je, Serikali inapokea ushauri kwamba, kodi hii ihamishiwe kwenye mafuta ili kurahisisha ukusanyaji wake na kuondoa kero kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, kodi hizi hutozwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge letu Tukufu. Kwa hiyo, kuifananisha na watumishi hewa siyo sahihi kabisa na ndiyo maana nimesema Serikali ina nia na imeanza maboresho ya sheria hii ili kuweza kuondokana na adha hii wanayoipata watumishi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kuifananisha kwa sababu ni ngumu kwa sababu ya jiografia ya nchi yetu. Huwezi tu kusema gari hii imesimama bila kujiridhisha kweli imesimama. Kama ilitolewa mjini na ikapelekwa Vijiji ambavyo hatuwezi kuvifikia, inakuwa ni tatizo kusema gari hili limesimama. Ndiyo maana nasema, naomba tuvute subira, tutakapoleta Finance Bill ya mwaka huu 2016/2017 anachokipendekeza Mheshimiwa Mbunge kitaonekana na adha hii itaondoka kabisa wala haitakuwepo tena kwa wananchi wetu.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa pamoja na upungufu uliopo katika kodi hii, lakini pia baadhi ya wananchi ambao sio waaminifu walikuwa wanatumia mwanya huo kutengeneza sticker ambazo ni feki: Je, Serikali ina mpango gani wa kuja na sticker madhubuti ambazo siyo rahisi kufojiwa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa wapo wananchi ambao wanatenda vitendo viovu vya kufoji sticker hizi. Kama nilivyosema, lakini naomba pia tufahamu kwanza Waheshimiwa Wabunge, katika sehemu ambako tumeboresha kwa kiasi kikubwa ni utoaji wa sticker hizi ambapo kwa sasa hivi mwananchi yeyote anaweza kulipia gari yake popote alipo na akaenda kuchukua risiti yake katika Ofisi zetu za Mamlaka ya Mapato popote pale alipo huku akiwa amepewa control number. Kwa hiyo, tumeweza kutoka katika manual work na sasa tunatumia teknolojia katika kutoa huduma hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maboresho hayo, kama nilivyosema, tusubiri Finance Bill itakapokuja, tutaona sasa kutakuwa hakuna mkono wa mtu yeyote kuingia katika ukusanyaji na utoaji wa sticker hizi kwa sababu itakuwa ni mfumo wa automatic ambao hakuna yeyote atakayeweza kuuingilia na kuweza kutoa sticker ambazo ni feki.
MHE. HASSAN S. KAUNJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nisikitike tu kwamba jibu lake haliendani na uhalisia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uhalisia uliokuwapo Lindi ni kwamba takwimu za watu wanaokadiriwa 100,000 ni wa Jimbo la Lindi Mjini. Vilevile nimkumbushe Naibu Waziri katika mchakato wa bajeti iliyopita ya mwaka jana kwamba maafisa wa Halmashauri walishakaa vikao tofauti na maafisa wa Wizara yake katika kuangalia uwezekano wa kubadili bajeti kutokana na idadi ya watu. Sasa anaposema kwamba idadi ya wakazi wa Lindi na akitumia takwimu za wapiga kura ni sahihi nakataa kukubali jibu lake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize maswali ya nyongeza kama tu Mheshimiwa Naibu Waziri na Wizara yake walikubali kwamba idadi ya watu wa Lindi ni kidogo na hivyo watafanyia kazi mchakato wa kuongeza bajeti katika bajeti inayokuja, je, yuko tayari kuthibitisha hilo au kulifanyia kazi hilo kwa bajeti inayokuja?
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kutokana na idadi ya watu kutotumika idadi stahiki katika Jimbo la Lindi imepelekea huduma za afya kupelekwa katika kituo kimoja tu cha afya katika Lindi Mjini na hivyo kupelekea shida kubwa kwa watu wa Lindi.
Je, Mhehsimiwa Waziri anayehusika yuko tayari kuiboresha hospitali inayotoa huduma ambayo inaendeshwa na Jeshi la Polisi Lindi ili kuweza ku-accommodate matatizo ya afya ya wananchi waJimbo la Lindi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiiwa Mwenyekiti, kwa swali la kwanza ambalo anasema kwa bajeti inayokuja, naomba nilikumbushe Bunge lako tukufu kwamba Bunge hili lilipitisha sheria ya takwimu Machi, 2015 ambayo inatoa mamlaka kwa Ofisi ya Taifa ya Takwimu kuratibu takwimu zote rasmi. Na kwa Serikali tunachofahamu ni kwamba idadi ya watu wa Lindi Mjini ni ambao wametajwa na kwa makadirio ya mwaka 2016, idadi ya watu Lindi Mjini ni 85,871 hiyo ndio takwimu rasmi inayotambulika na Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuhusu swali la pili, naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge swali hili tutakaa pamoja na Waziri wa Afya na Waziri wa TAMISEMI tutalifanyia kazi kuona hospitali hii inaboreshwa.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa kuwa, kumekuwa na ubadilishanaji wa fedha kiholela sana hasa katika sehemu za mipaka yetu na nchi jirani. Mfano, kama kule Tunduma ambapo ubadilishanaji huu huwa kama vile tunagawiana njugu yaani holela. (Makofi)
Je, Serikali ina mkakati gani wa kurasimisha kazi hii inayofanywa na watu wa kawaida na kuweza kuchukuliwa na Serikali ili kuwaondoshea hata wale watu wanaofanya kazi hiyo, inawezekana hata wakapoteza maisha yao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Serikali haioni kwamba inapata hasara na haipati mapato mengi ikiachia biashara hii iendeshwe isivyo halali?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Faida Mohamed Bakar kwa umakini wake katika ufuatiliaji wa masuala ya kifedha na uchumi wa Taifa letu. Serikali inakiri uwepo wa watu wanaojihusisha na biashara hii kiholela hasa katika mipaka mbalimbali ya nchi yetu na nchi jirani, kwa mfano, kule Tunduma kama alivyosema, Namanga, hata pia katika Miji yetu mikubwa kama Arusha na Mwanza, lakini Serikali yetu haipo kimya katika kulishughulikia tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kupitia Sheria yetu ya Fedha za Kigeni ya Mwaka 1992 na Kanuni tulizozipitisha mwaka 2015, Serikali inaendelea kushughulikia tatizo hili. Pia, tunakiri kwamba, mapato ya Serikali yanapotea ndiyo maana Benki Kuu pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi wamekuwa wakiendesha operation na warsha mbalimbali katika sehemu hizi nilizozitaja ili sasa kuwasaidia wananchi wetu hawa kuwa na uelewa wa hatari ya biashara wanayofanya, pia na kuonesha kwamba, ni kwa jinsi gani Taifa letu linapoteza mapato katika eneo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba, tunatambua hili na tumeendelea kutoa warsha katika maeneo haya na kwa watu hawa tunafanya jitihada za hali ya juu kuhakikisha sasa watu hawa wanarasimishiwa biashara zao hizi wanazozifanya, ili kwanza kama alivyosema Mheshimiwa Faida, kupunguza hatari ya maisha yao na pia kuhakikisha Serikali yetu inapata mapato ambayo tumekuwa tunapoteza.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa fursa hii na nimshukuru Mheshimiwa Faida kwa swali zuri alilouliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la msingi linahusu matumizi ya dola, hivi sasa kumekuwa na kilio cha wanafunzi wengi wa vyuoni kulipishwa ada kwa malipo ya dola na baadhi ya taasisi, ikiwemo taasisi hii ya TRA inayoongozwa na Waziri na Naibu Waziri wa Fedha. Je, kuna Sheria yoyote iliyopitishwa humu kuhusu suala hili na amesema tokea 1992 hakuna utaratibu huo? Je, hatua gani zinazochukuliwa kwa taasisi hizi zinazolipisha ada ya dola kinyume na sheria?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekiri na nimesema kwamba, tunafahamu zipo taasisi zinazotumia dola katika kufanya transaction. Nimesema pia, ni mojawapo ya chanzo cha Serikali yetu kupata fedha za kigeni moja ya faida ni hiyo, lakini kama nilivyosema ni asilimia 0.1 tu ya transaction zinazofanyika nchini zinazotumia dola ya Kimarekani. Kama nilivyosema Sheria ilipitishwa na Kanuni zake zimepitishwa mwaka 2015.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba tunawachukulia hatua gani, bado hatuoni kwamba, inahatarisha na kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, siyo sababu inayopelekea thamani ya pesa yetu kupungua.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yasiyotosheleza sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. (Makofi)
Swali la kwanza; kwa kuwa kutunza dhahabu kwenye hazina ya nchi yoyote ni kuashiria utajiri wa nchi hiyo; kwa mfano, nchi ya Marekani ina dhahabu zaidi ya tani 8,100 kwenye hazina yake, lakini nchi ya Ujerumani 3,300 na nchi ya Italia ina tani 2,450. Kwa nini Tanzania tunachelea chelea kutunza dhahabu wakati sisi sasa hivi ni wazalishaji wa dhahabu duniani?
Swali la pili, kwa kuwa Tanzania ni nchi inayozalisha dhahabu kama Ghana, ina tani nane kwenye ghala yake, lakini Afrika ya Kusini ina tani 125. Na kwa kuwa kwa kipindi cha muda mrefu dhahabu imekuwa ikipanda thamani. Miaka ya 1900 dhahabu ilikuwa zaidi ya dola 200, miaka ya 2000 ilikuwa zaidi ya 500; sasa hivi ni zaidi ya dola 1000. Kwa nini Serikali inachelea kwamba dhahabu inatelemka bei. Kwa nini sasa Serikali isifanye utafiti ikaangalia nchi zingine zinafanyaje na ikatunza dhahabu kwenye hazina yake kwa ajili ya kupandisha uchumi wa nchi yetu? Ahsante sana.
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza, sababu kubwa ya msingi ya Benki Kuu ya nchi yoyote kuweka akiba yake katika dola ni kujiwekea akiba (reserves), hiyo ndiyo sababu ya msingi ya Mataifa yote. Hata katika historia wakati wa vita, dhahabu ilichukuliwa kama mkivamia nchi moja kitu cha kwanza mnachokimbilia kuchukua kwa wale mliowashinda mnachukua ile dhahahu kwa sababu ina hesabika ndiyo inabeba thamani ya vitu. Kwa hiyo, sana siyo kuonesha kiwango cha utajiri katika nchi kama sababu ya msingi ya kuweka akiba yako katika dola. Vilevile tunachelea kuweka akiba yetu katika dola kwa sababu ya msingi….
Mheshimiwa Spika, tunachelea kuweka akiba yetu katika dhahabu kwa sababu ya tabia ya bei ya dhahabu katika miaka ya karibuni kama Mheshimiwa Naibu Waziri alivyoeleza.
Mheshimiwa Spika, hata huko Ghana ambako ni kweli wana akiba ya dhahabu ya tani 8.4 ambayo siyo sehemu kubwa sana ya akiba yao ya reserves na wamekuwa na akiba hiyo toka mwaka 2000, kiasi hicho hakijabadilika. Hali kadhalika Afrika ya Kusini toka mwaka 2016 wamebakiwa na tani 123.8 tu na kiasi hicho kimeteremka na kufikia tani 183.1, lakini ni wasiwasi huo wa mwenendo wa bei ya dhahabu katika soko la dunia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa hivi Serikali inafanya uchambuzi kuona uwezekano kama tunaweza tukaweka sehemu yetu ya akiba katika Tanzanite badala ya dhahabu lakini hii ni kazi ambayo inaendelea.
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini swali langu la msingi niliuliza ni utaratibu gani mtaweza kuwasaidia makundi maalum ya wanwake na vijana ili waweze kupata mikopo kwa riba nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili nilitaka kuuliza, kwa kuwa kuna ugumu na sheria zinazoibana Serikali kusimamia riba hizi. Ni lini sasa Serikali itatusaidia kutimiza ile ahadi ya shilingi milioni 50 kila kijiji na mtaa ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu na kinamama wa Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi; kwa mujibu wa Sheria Benki Kuu haiwezi kutoa maelekezo ya kuleta riba elekezi ili kuweza kusimamia mabenki haya yaweze kufanya vizuri katika soko letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuhusu shilingi milioni 50 kama ambavyo Serikali imekuwa ikisema; tunaendelea kuandaa utaratibu na kwenye bajeti yetu ya fedha ya mwaka 2016/2017 tumetenga bajeti hii na tutaweza kuitekeleza kabla ya mwaka huu wa fedha haujaisha.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa jibu la msingi la Mheshimiwa anasema Benki Kuu haiwezi kuingilia kutoa bei elekezi, tunawezaje kusaidia Benki ya Wanawake iweze kutoa riba ndogo kwa kupata ushauri kutoka kwenye Wizara yake?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema mwanzo, kwa mujibu wa sheria Benki Kuu haiwezi kutoa hiyo riba elekezi na napenda niseme kwamba riba hizi zilizopo ni kwa mujibu wa Sera ya Riba ya mwaka 1992. Kwa hiyo, lazima tuendane na sera tuliyoipitisha humu Bungeni ili kuweza kuhakikisha kwamba sekta ya fedha inafanya vizuri ndani ya uchumi wetu na kwa Benki ya Wanawake naamini Mheshimiwa Waziri wa Afya anaweza kulisimamia hili na kuweza kutoa riba ambayo ni nzuri, lakini hawezi kukiuka misingi ile iliyowekwa na Sera ya Riba ya mwaka 1992.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika siku za hivi karibuni tumeshuhudia leseni za kufanya biashara katika Manisapa mbalimbali zinatolewa baada ya kupatikana kwa tax clearance, lakini ukweli ni kwamba sio biashara zote hasa biashara ndogo zinahitaji wakati mwingine tax clearance, haioni ni wakati muafaka kuweka categories za biashara ambazo wanaweza kupewa leseni bila hata tax clearance badala ya kinachofanyika sasa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hili ni swali la kutoa leseni ambalo ni swali jipya ambalo tumeondoka katika riba, kwa hiyo naomba niseme tu tuna viwango ili kuweza kutoa leseni katika biashara zote zinazoendeshwa ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, kama hawajafikia ndani ya kiwango kile kinachohitajika mfanyabiashara huyo wala hatozwi na wala hapewi leseni lakini akishavuka yale malengo ya biashara yake tayari anatakiwa apewe leseni na tunasimamia kama moja ya njia za kukusanya mapato yetu.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Pamoja na mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kuwezesha elimu bure, upatikanaji wa madawati na pia watumishi hewa kuondolewa, naomba kufahamu, kwa sasa Watanzania wengi hasa akinamama katika SACCOS zao wamekuwa na hamu kubwa ya kufanya biashara. Je, Serikali inachukua hatua gani kuwezesha SACCOS za akinamama katika halmashauri zote zipate hela za kutosha?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ikumbukwe kwamba sote humu ndani Waheshimiwa Wabunge sisi ni Wajumbe katika Mabaraza yetu ya Halmashauri, hivyo tunatoa asilimia tano katika mapato ya halmashauri na hayo ni katika kuimarisha vikundi vyetu vya VICOBA pamoja na SACCOS zilizopo ndani ya halmashauri zetu. Nitoe wito tu kwa Waheshimiwa Wabunge, tusimamie kwa ufasaha asilimia hizo tano za mapato ndani ya Halmashauri zetu ili ziweze kuwafikia wananchi wetu hasa akina mama na vijana ili kuweza kuinua uchumi wao.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa kituo hiki kilipoanzishwa mwaka 1989 tayari Tanzania ilikuwa na Ubalozi Mjini London ambao ulianzishwa mwaka 1961, na moja ya jukumu la kituo hiki ni kuvutia uwekezaji na hasa suala la utalii ambao unachangia asilimia 17.5 ya Pato la Taifa. Je, nini kilionekana kimeshindikana wakati huo kufanywa na Ubalozi na ambacho sasa kinaweza kufanywa na Ubalozi huo?
(b) Kwa kuwa kituo kimefungwa na miongoni mwa madai makubwa ambayo Serikali ilikuwa inadaiwa ni posho za wafanyakazi wa kituo waliopo London, mishahara ya wafanyakazi na kodi za nyumba za wafanyakazi wetu waliopo London.
Je, Serikali inaweza kutoa tamko gani juu ya madai ya wafanyakazi wa kituo hiki waliopo London kama wameshalipwa fedha zao na kama wamerejeshwa nchini, je, wamelipwa fedha zao za kujikimu?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema yalikuwa ni maagizo ya Mheshimiwa Rais lakini pia naomba ikumbukwe kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imesema na inatekeleza sasa kuboresha na kupeleka watumishi wote katika balozi zetu zote duniani ili kuhakikisha wao wanafanya kazi husika na zinazostahiki kufanywa na balozi setu.
Kwa hiyo agizo lile halikuwa la makosa na sasa Serikali ya Awamu ya Tano imerejesha jukumu hili ndani ya Ubalozi ambalo ni moja ya majukumu yake na Ubalozi wetu unaendelea kufanya vizuri.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, niseme kama Naibu Waziri wa Fedha, madai tuliyoyapata ni shilingi 129,896,000 na ndiyo ambayo tunayalipa kama kuna watumishi ambao wanadai posho zao na haki zao zozote naomba watuletee ili tuweze kuhakiki na tutaweza kulipa kama ambavyo tumelipa deni lililotangulia.
MHE. ENG. ATASHASTA J.NDITIYE: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru sana, jina langu ni Atashasta Justus Nditiye au Engineer Nditiye inatosha. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wawekezaji wazawa Green Field Plantations walianza mchakato wa kufuatilia eneo hilo toka mwezi wa pili mwaka jana na tuliwapa ushirikiano namshukuru sana Mkuu wa Wilaya pamoja na wananchi wa Jimbo la Muhambwe, lakini ilipofika mwezi wa nane ameondoka mpaka sasa hivi ninapoongea hajarudi. Tunadhani ni muhimu sana tupate mwekezaji competitor kwa ajili ya ku-speed up suala la yeye kuja kufanya shughuli za uwekezaji kama tunavyotarajia ili wananchi wasije wakakata tamaa. Ni lini Serikali inafikiria kutafuta mwekezaji mwingine ikiwezekana hata wa kutoka nje ili kuweza kuwekeza katika Kiwanda cha sukari? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika kuelekea kwenye sera ya viwanda katika nchi yetu tuna wabunifu wengi sana na katika Wilaya yetu ya Kibondo kwa mfano, kuna kijana amebuni magodoro yanayotumia mifuko ya plastic na kila alipojaribu kuwasiliana na COSTECH kwa ajili ya ushauri wamekuwa hawampi ushirikiano wa kutosha. Ni lini Serikali inajipanga kuwaongezea uwezo COSTECH ili wanapopata maswali kutoka kwa wabunifu wadogo wadogo waweze kuwatembelea na kuwapa ushauri? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata taarifa kwamba hapa mwekezaji aliondoka na hajarejea na kama alivyosema Serikali yetu ya Awamu ya Tano ni Serikali ya viwanda. Tutamleta mwekezaji mwingine kama alivyosema na siyo mmoja bali wawili, watatu kuongeza competition na ufanisi hilo nimelichukua na Serikali inalifanyia kazi, watakuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ubunifu na COSTECH; kwanza nikiri kwamba huyo mwanafunzi na nimwambie Mheshimiwa Mbunge mwanafunzi huyo ni mwanafunzi wangu niliyemfundisha Masters Chuo Kikuu Mzumbe. Namfahamu na tulimfundisha na sasa anaendelea na ubunifu huo na COSTECH pamoja na Chuo Kikuu Mzumbe tumepanga kumuendeleza mwanafunzi huyo pamoja na wabunifu wote wanaoibuka ndani ya Nchi yetu.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Niongezee kwa hoja ya msingi iliyozungumzwa. Mwekezaji huyo katika Bonde la Malagarasi aliyeko Muhambwe pia yuko mwekezaji mwingine anaitwa Kigoma Sugar yuko Bonde la Malagarasi upande wa Wilaya ya Kasulu. Wote hawa inaonekana wameshindwa na kama sisi Kasulu tunataka ardhi yetu ekari 100,000 tumnyang‟anye sasa tuweze kutafuta mwekezaji mwingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilikuwa naomba basi juhudi hizo za kutafuta mwekezaji zifanyike kote Muhambwe na Wilaya ya Kasulu kwa sababu wote wako kwenye Bonde hilo la Malagarasi. Kwa hiyo, swali langu ni kuomba tu Serikali wawekezaji wote hao wa zamani wameshindwa, hawapo.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme siyo kwa Wilaya ya Muhambwe na Kasulu tu, niseme kwa Wilaya zote na maeneo yote ya uwekezaji na hasa uwekezaji kwa ajili ya kilimo cha miwa pamoja na viwanda vya sukari. Naomba tupatiwe taarifa ili Serikali tuchukue hatua mara moja kama walipewa ardhi basi naamini Waziri wa Ardhi yupo makini tutaichukua ardhi hiyo na kumpa mwekezaji mwingine.
Kwa hiyo, niombe Waheshimiwa Wabunge tupate taarifa ya wawekezaji wote wanaonekana ni wababaishaji na wameshindwa kufanya kazi, tushirikiane na Tanzania ya viwanda inawezekana.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri. Pamoja na Tanzania kwamba tuna maeneo mengi mazuri kwa ajili ya kilimo cha miwa na viwanda tulivyonavyo vya sukari na pamoja na mbwembwe nyingi za Serikali ya Awamu ya Tano iliyonazo kukuza uchumi, lakini bado bei ya sukari katika nchi yetu ni kubwa sana na uwezo wa wananchi wetu ni mdogo. Je, ni lini Serikali itaangalia sasa uwezekano wa kupunguza bei ya sukari ili ifikie angalau pale tulipokuwa na tatizo la sukari wananchi wetu waweze kumudu kununua sukari?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikanushe Serikali ya Awamu ya Tano siyo ya kibabaishaji tunafanya kazi na kama alivyosema Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa tathmini ya mwezi Januari viwanda vyetu vya ndani vimeshazalisha asilimia 86 ya uhitaji wa sukari ndani ya nchi yetu, kwa hiyo, ninauhakika kwa demand na supply nguvu hii tayari tukishaweza kuzalisha asilimia mia moja bei ya sukari itashuka. Tukumbuke tu Waheshimiwa Wabunge nchi hii ni huru na inafuata soko huria, hatuwezi kuingilia hilo na turuhusu sasa Viwanda vyetu viweze kuzalisha asilimia mia moja na bei ya sukari itashuka na wananchi wetu watafurahia Serikali yetu ya Awamu ya Tano utendaji wake.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na
majibu ya Waziri, Manispaa ya Iringa ina miradi mikubwa ya Machinjio ya Kisasa
ya Ngelewala, Soko la Ngome, Sekondari ya Mivinjeni, Nyumba za Waganga na
Wauguzi wa Zahanati ya Njiapanda na Nduli. Katika Baraza la Madiwani, kupitia
bajeti ya mwaka 2016/2017, Manispaa ya Iringa ilikadiria kukusanya mapato ya
ndani Sh. 4,532,000,000 ili kuweza kumalizia miradi midogo iliyokuwa inaikabili
Manispaa hiyo. Manispaa ya Iringa, vyanzo vikuu vya mapato vinatokana na
kodi ya majengo, Serikali ikaamua kodi hizi za majengo zikusanywe na TRA, je, ni
lini Serikali itaona umuhimu wa kupeleka hela za miradi hii kwa wakati ili kuweza
kumalizia miradi ambayo haijamalizika hadi sasa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika,
napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba Serikali inaona umuhimu wa
miradi yote ya maendeleo kama ilivyopitishwa katika bajeti yetu mwezi Juni.
Hivyo, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, kinachopelekea kupeleka
fedha hizi ni upatikanaji wa fedha hizi. Kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge
ameongelea kuhusu kodi ya majengo, naomba nimwambie kwamba TRA
imekusanya kodi ya majengo mwezi wa Kumi, baada ya quarter ya kwanza
kupewa Halmashauri zenyewe kukusanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge,
anapuhudhuria Baraza la Madiwani aweze kusimamia mapato yaliyopatikana ili yaweze kutumika katika miradi aliyoitaja. Serikali yetu baada ya kukusanya
kuanzia mwezi wa Kumi, fedha zote tulizoahidi zitarejeshwa katika Halmashauri
husika kutokana na bajeti zilizopitishwa.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Namshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake ambayo hayatoshelezi kwa
sababu niliwahi kuuliza swali hili lakini nimepata majibu yale yale.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la msingi, ni kwa nini tuendelee
kutumia dola katika kununua, siyo uhuru wa soko. Sasa swali la kwanza, kwa nini
Tanzania isitumie utaratibu wa nchi zingine kama Zambia, South Africa, Ghana,
Dubai na Ulaya? Wote tumesafiri tumeona ukifika tu kwenye nchi hizo
unaachana na matumizi ya dola lazima ubadilishe na ukalipe kwa hela yao.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa nini au ni lini Serikali sasa
itakagua haya maduka ya fedha ambayo kwa kweli kuna taarifa za ki-intelijensia
zinasema wanatumika kutorosha fedha zetu? Wakaguliwe, mapato yao
yajulikane na ijulikane pia ni jinsi gani wanazitumia hizi fedha na kuziweka kwenye
soko letu la Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la
kwanza, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi Sheria yetu ya Benki Kuu ya
mwaka 2006, Sehemu ya Tatu, kipengele cha 26 kimeweka wazi kabisa kwamba
fedha halali kutumika ndani ya nchi yetu ni shilingi ya Kitanzania. Pia Sheria ya
Usimamizi wa Fedha za Kigeni ya mwaka 1992 inaruhusu mtu yeyote kupokea na
nimeeleza kwa nini Serikali yetu imepitisha sheria zote mbili, dhamira ikiwa ni
kukuza uchumi wetu na kuwa na fedha za kigeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwambie tu Dokta Kafumu
kwamba nchi nyingine hufuata utaratibu kutokana na mazingira ya nchi yao.
Kwa nchi yetu hatujaona athari kubwa ya kuruhusu wageni wetu kutumia fedha
hizi ndani ya uchumi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, ni lini Serikali itakagua, naomba
nimwambie kwamba, Serikali yetu inakagua siku hadi siku. Kama nilivyosema
katika jibu langu la msingi Serikali yetu haijalala, Benki Kuu kwa kushirikiana na
Mamlaka ya Mapato zinakagua siku hadi siku na sasa miamala yote ya maduka
haya ya kubadilishia fedha yanakuwa monitored na Benki Kuu kupitia TRA. Pia
tunaendelea kuimarisha mifumo yetu ili kuhakikisha fedha na uchumi wetu uko
salama kabisa.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri, nitakuwa na maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa mashaka ya vijana wetu yamekuwa yakizidi siku kwa siku, vijana wanajihusisha katika michezo hii ambapo muda mwingi unapotea hata muda wa masomo, muda wa kufanya kazi …

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Maadili yamepotea, kuna masuala ya betting ambayo yanachukua muda mwingi wa vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Waziri kuniambia kwamba kuna Sheria Namba 4 inayoruhusu mambo hayo lakini udhibiti wake ukoje? Je, mpaka sasa ni wafanyabiashara wangapi wamekamatwa na maduka yao kufungwa ambao hawakuzingatia taratibu za kuzuia vijana wenye umri mdogo kuingia sehemu hizo na je, wamepelekwa kwenye vyombo husika na kuchukuliwa hatua?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza aliuliza udhibiti wake ukoje, kama nilivyosema sheria yetu imeweka wazi na Bodi ya Michezo ya Kubahatisha iko makini kusimamia michezo hii yote ndani ya nchi yetu ili kuhakikisha sheria hii iliyotungwa na Bunge letu Tukufu inafuatwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, ni watu wangapi na maduka mangapi yamefungwa, naomba nilichukue swali hili tuweze kulifanyia kazi kwa sababu linahitaji data mahsusi ili tuweze kumjulisha Mheshimiwa Mbunge pamoja na Bunge lako Tukufu.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Napenda na mimi nimuulize Naibu Waziri swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa hii michezo ya kamari imekuwa ikichezwa kwenye stendi kubwa na sehemu za starehe na kupelekea watu kufilisika na wengine kufikia hatua hata ya kujiua. Je, hamwoni sasa ni wakati muafaka wa kukataza michezo hii isichezwe na wale wanaochezesha michezo hii wachukuliwe hatua?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema michezo hii ipo kisheria, sisi kama Wizara hatuwezi kuisitisha. Tutafanya utafiti ili tuone kama inahitajika kuleta sheria mpya Bungeni ili tufanye hivyo. Hata hivyo, tusisahau kama nilivyosema michezo hii ni sawa na michezo mingine pale inaposimamiwa vizuri na sisi tuna uhakika inasimamiwa vizuri. Kwa mfano, kwa mwaka jana 2016 mchezo huu ulichangia zaidi ya shilingi bilioni 2.1 katika mapato yetu. Hivyo, niombe tu kama jamii na kama Taifa tuweze kuwasimamia vizuri vijana wetu ili yale madhara hasi yasiweze kupatikana.
MHE. MACHANO OTHMAN SAID: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha, naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ni kwamba kutokana na kwamba hii Sheria ya Fedha ipo kwa muda mrefu tangu mwaka 1991, na kutokana na mabadiliko ya kidunia ya uchumi na baadhi ya nchi jirani kubadilisha sheria hizi katika nchi zao; je, haaoni kwamba umefika wakati kwa Serikali kubadilisha sheria hii?
Na la pili, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba riba katika mwezi wa Juni, 2016 ilikua kwa kiwango cha 13.46 lakini ukweli halisi ilikuwa ni kati ya 16 mpaka 18. Katika swali langu niliuliza je, haoni kwamba Serikali inahitaji ichukue juhudi maalum kwa wafanyakazi wa Serikali kwa sababu fedha zao kulipwa ni rahisi na zina dhamana zaidi, anaonaje Mheshimiwa Waziri?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza anauliza utayari wa Serikali kubadilisha sheria, naomba nilikumbushe Bunge lako Tukufu, tuko katika soko huria na tunafuata soko huria hivyo haiwezekani kurudi katika kuelekeza mabenki yetu. Kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, Benki Kuu ikifanya hivyo itakosa mamlaka sasa ya kuyasimamia mabenki hayo pindi yatakapopata hasara kutokana na riba elekezi iliyoyatoa. Hivyo nashauri tu tuendelee na mfumo uliopo kwa sababu tupo katika mfumo wa soko huria na hii pia ni global practice hivyo siamini kwamba ni njia njema kwa nchi yetu kuweza kurejea katika maelekezo kwa ajili ya riba zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, naomba niseme kwamba kuhusu kutoa riba elekezi kwa wafanyakazi pia haiwezekani kwa sababu riba tunazoziona zinakuwa ni wastani wa riba ambazo zimetolewa kutoka katika sekta na makundi mbalimbali, hivyo tukisema wafanyakazi tuwape riba nafuu itapelekea makundi mengine ambayo hasara yake au vihatarishi ni vya juu kupata riba kubwa sana na hivyo tutakuwa tumewaumiza.
Kwa hiyo, niliombe Bunge lako Tukufu na Wabunge kwamba tukubaliane na wastani huo ambao hutolewa na Benki Kuu baada ya kupata sasa riba zote kutoka katika mabenki yetu yote.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, na mimi naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa wajasirimali wadogo wadogo hasa mama lishe na wamachinga na ambao wengine wana vipato vya chini wamekuwa wakikopa mikopo kwa ajili ya biashara zao na kutozwa riba kubwa na kushindwa kurejesha mikopo ile na kufilisiwa.
Je, Serikali ina mikakati gani kuhakikisha inatafuta fedha kwa ajili ya Wajasiriamal wadogo wadogo na kuwatoza riba ambayo inaendana na biashara zao?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nilikumbushe Bunge lako tukufu kwamba tayari Serikali imeshatunga sera ya huduma ndogo za fedha za mwaka 2016 na sasa tupo katika hatua nzuri kuja na sheria katika Bunge lako tukufu ili kuwalinda wajasiriamali wadogo wanaokopeshwa kwa riba kubwa. Ni imani yangu sheria hii itakapokuwa imepitishwa watakopa katika viwango halisi ambavyo viko sokoni na sivyo ambavyo wanaonewa kwa sasa.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia fursa hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza pamoja na majibu aliyonipa Mheshimiwa Waziri lakini sikuridhika na majibu haya.
Mheshimiwa Waziri katika majibu yake ya msingi anasema kwamba kati ya bidhaa ambazo hazitozwi kodi pamoja na vinyago, lakini katika swali hilo hilo la msingi anabainisha kwamba kati ya vitu vinavyokamatwa na kupigwa mnada ni pamoja na vinyago. Mheshimiwa Waziri katika suala hili ulivyolijibu huoni kwamba umejichanganya? Kama vinakamatwa na kupigwa moto, vinakamatwa kwa kosa lipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kuuliza swali la pili, je, Serikali imetoa elimu yoyote kuhusiana na suala zima la uuzaji wa vinyago kwa wajasiriamali wadogo wadogo ukizingatia Mheshimiwa Rais ameondosha kodi ndogo ndogo kwa wajasiriamali?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, naomba nikiri kwamba sijamchanganya, vinyago tunafahamu ni bidhaa zinazotokana na maliasili za nchi yetu hivyo inawezekana watu wa Wizara ya Maliasili wanatozo zao ambazo wanazitoza. Mimi nimekanusha utozaji wa kodi ambao tunatoza sisi kama Wizara ya Fedha kwamba hizi hazipo katika orodha ya bidhaa tunazozitoza kodi (extport duty). Kwa hiyo, ndiyo maana katika jibu langu la sehemu ya pili nilisema yawezekana zilikuwa zinatakiwa kulipiwa tozo mbalimbali kutoka katika Wizara ya Maliasili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, elimu ya ujasiriamali tunaendelea kuitoa, kuna kitengo ndani ya Wizara yangu ya Fedha na tunaendela kuifanyia kutoa elimu ya ujasiriamali kwa wajasirimali wote nchini wakiwepo wafanyabiashara wa vinyago.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kutokuwa na afya naomba kuuliza maswali mawili madogo
ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri kuna ushahidi ambao kama utakuwa tayari kuja kuueleza kuwa kuna kodi zinalipwa Bara, je, utakuwa uko tayari kupokea ushahidi huo ili Zanzibar nayo inufaike kibiashara kupata mapato hayo ili imalize deni lake la umeme inayodaiwa? (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuna Tume ya Fedha iliyoundwa mwaka 2007 mpaka leo hiyo Tume ya fedha haijakutana kutatua matatizo hayo, je, ni lini kama Naibu Waziri utachukua hatua hizo ili kutatua tatizo hili la Tume ya Fedha ya Pamoja iliyoundwa nafikiria mwaka 2007 hadi
leo karibu miaka 16 haijakutana?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ipo tayari kabisa kupata huo ushahidi anaosema na ikiwa tutajiridhisha ni kodi iliyotakiwa kukusanywa Zanzibar imekusanywa Bara tuko tayari kuirejesha Zanzibar, kwa hiyo, naomba tupate ushahidi huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Tume ya Fedha ya Pamoja najua imeundwa kama alivyosema na inafanya vikao vyake sasa pia nimeshangaa kusema kwamba tangu imeundwa haijawahi kufanya kazi. Nalichukua suala hili na kama Serikali tunalifanyia kazi.
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Tunaipongeza Serikali kwa kukusanya kodi kwa kiwango ambacho ni cha juu sana, lakini wafanyabiashara wanatakiwa wajikisie makisio yao na ndio walipe kodi kutokana na vipengele ambavyo wameweka kwenye makisio.
Je, Serikali ina kauli gani juu ya malalamiko yaliyoko sasa hivi kwamba watumishi wa TRA wanakisia zaidi ya yale makisio ambayo wao ndio wanatarajia kufanya mauzo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na malalamiko hayo kuhusu watumishi wetu wa TRA na tumekuwa tukifanya vikao kuhusu suala hili. Naomba kuliharifu Bunge lako tukufu kwamba pia
kumekuwa na tatizo la wafanyabiashara zetu kuleta taarifa ambazo sio sahihi ndio maana inapelekea kupata mvutano kati ya wafanyakazi wetu wa TRA na wafanyabiashara. Lakini kama Serikali tunasimamia uadilifu na kwa uhakika kabisa kinachotendeka ndani ya TRA ni kitu ambacho kinasimamiwa kwa maadili, sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Jibu la msingi la Mheshimiwa Waziri amesema kwamba kodi hizo zinalipwa kwa kigezo cha usajili. Ukweli ni kwamba kampuni zote zinasajiliwa kutokana na headquarter alipo regulators. Kwa hiyo, mabenki mengi na makampuni ya simu yako Bara na regulators wake wako Bara, usajili wake unafanyika Bara wanalipia Zanzibar. Lakini ukweli upo kwamba mkaa na maiti haachi kulialia na mtegemea nundu haachi kununa, je, Serikali iko tayari kutumia kigezo cha operations za hizi kampuni kodi ikawa-charged kule ambapo zina-operate?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kodi ambayo tunaiita corporate tax inalipwa kule ambako kampuni imesajiliwa. Hilo alilolisema Mheshimiwa Ali King ni
sahihi lakini pia naomba ndugu zangu tuweze kuangalia uhalisia ulivyo. Kwa mfano makampuni makubwa kama Kampuni ya Bakhresa, Kampuni ya Zanzibar Insurance, Kampuni ya Zantel zimesajiliwa Zanzibar na kodi ya mapato inalipwa kule Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hicho anachokisema naomba nimwambie Mheshimiwa Ally King kwamba hata hizi ambazo zinakusanywa kule Zanzibar, zinakusanywa huku Bara kwa pamoja zinaingia katika mfuko mkuu wa Serikali na kwa pamoja fedha hizi zinapoingia kwenye mfuko mkuu wa Serikali tunaweza pia kuhudumia
Serikali zote za pande mbili ya Bara na Zanzibar.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la fedha kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa sasa ni donda ndugu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mabadiliko ya Sheria ya VAT ya mwaka 2014 kama sikosei imepitishwa kwamba bidhaa zinazotoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar hazitozwi ushuru hapa Tanzania Bara na wanatakiwa watoze ushuru kule Zanzibar ambako ZRB wanatoza ushuru wa asilimia 18. Lakini bado TRA Zanzibar wanawatoza wafanyabiashara hawa trade levy ya asilimia tano kusema kwamba bidhaa ile ile mfanyabishara wa Zanzibar anatakiwa ailipie asilimia 23 ya kodi, je, huku si kumuonea mfanyabiashara huyu wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo ameanza yeye mwenyewe kusema Sheria ya VAT tuliipitisha hapa na tunaitekeleza kisheria. Hilo analolisema la wafanyabiashara kwamba wanaonewa nimuombe Mheshimiwa Mbunge kama na yeye ana uthibitisho wa hilo analolisema aweze kutupatia ili tuweze kufanyia kazi. Lakini kitu ambacho kipo tunajua kodi zote zinatozwa kulingana na sheria zilizopitishwa na Bunge lako
tukufu.
MHE. DEO F. NGALAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Jumuiya ya Afrika Mashariki ilivunjika mwaka 1977, mpaka
leo hii ni miaka 40. Shirika hili limekuwa likisuasua sana lakini moja kati ya vigezo inavyolifanya lisuesue ni kwamba hela yake ambayo ilitakiwa iingie kwenye operesheni ndiyo hiyo ambayo inatumika kuwalipa wale wastaafu wa Afrika Mashariki. Je, Serikali ina mpango gani sasa hivi kuanza kuwalipa wale wastaafu yenyewe moja kwa moja bila kutumia fedha za shirika? Pili, fedha hizi ambazo tayari Shirika la Posta linaidai Serikali ni lini zitakamilishwa kulipwa kwa sababu imefikia kipindi Shirika linasuasua, ikafikia kipindi hata ule mwaka 2016 Shirika hili lilifungiwa akaunti zake kwa sababu TRA ilikuwa inalidai sh. 600,000,000. Je, kulikuwa na fairness gani ya kufungia zile hela wakati shirika hilo linaidai Serikali shilingi bilioni tano?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza Serikali ina mpango gani wa
kulipa yenyewe, naomba kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba Serikali sasa hivi iko kwenye jitihada za kuhakikisha kuwa malipo haya yanalipwa na Serikali yenyewe na kwa kuwa tayari watumishi wote wa Shirika la Posta wanaendelea kuchangia kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, wastaafu hawa wataendelea kulipwa na Mifuko hii badala ya kulipwa tena na Shirika la Posta.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni lini fedha hizi zitalipwa. Kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba, tutaendelea kulipa kwa kadri fedha zinapopatikana na ni jukumu la Serikali kulipa fedha hizi tunafahamu, tumejipangia mpango itakapofika Juni 30, shilingi bilioni 3.2 zote zitakuwa zimeshalipwa.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Hapo kwenye hilo swali, napenda kuiuliza Serikali wapo wastaafu kule kwangu wengi zaidi ya 20 ambao wananifuata ofisini, ni wazee, wengine wameshafariki hawajalipwa waliokuwa watumishi wa Afrika Mashariki, waliokuwa watumishi kama Game Officers. Sasa kwa nini Serikali isiwe proactive kuwafuatilia hao wazee huko waliko ili waweze kulipwa mafao yao, badala ya kutusumbua Wabunge ambao tumeingia hivi karibuni?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo Watanzania wote ni mashahidi, Wizara ya Fedha na Mipango ina zaidi ya miezi mitatu sasa ikizunguka mikoa mbalimbali kufanya tathmini na kuhakiki wastaafu wote. Kwa hiyo, hilo alilolisema Mheshimiwa Kakunda, Wizara ya Fedha ilishafika Tabora na tayari imeshafika Sikonge. Kama wapo ambao hawakufikiwa tuna utaratibu zoezi hili ni endelevu waweze kufika na kuhakikiwa na haki yao watapata bila tatizo.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na majibu ya Serikali hususan Wizara ya Fedha kwamba wastaafu wote wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki walishalipwa mafao yao. Hapa nina check ya mzee mmoja ambaye anaitwa Mzee Malembeka na Mheshimiwa Naibu Waziri unamfahamu, katika madai yake alikuwa anadai shilingi milioni 15 Serikali imemlipa shilingi milioni tano tu. Sasa na hapa ni wazee wengi sana, naomba kauli ya Serikali.
Je, ni kweli kwamba wazee wastaafu wote wa Afrika Mashariki wamelipwa fedha zao na kwamba hawaidai Serikali? Atoe tu tamko ili tujue hili jambo limekwisha au bado wazee hawa wanaidai Serikali.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge lako Tukufu linajua ilishatolewa kauli ya Serikali ndani ya Bunge hili kuhusu malipo ya wastaafu wa Afrika Mashariki kwamba wastaafu wote walishalipwa. Kama nilivyosema hiyo ndiyo kauli ya Serikali iliyotolewa ndani ya Bunge hili, tulishafungua milango mtu ambaye anaona hajalipwa ana udhibitisho Wizara ipo tayari kumpokea na tuweze kuhakiki na kumlipa malipo yake.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri lakini naomba nimuulize. Hivi kwenye habari ya wagonjwa haya mambo ya kodi yanatoka wapi jamani kwenye magari yao? Kwa sababu hiyo sio biashara ni huduma. Kwa hiyo, naomba aniambie hiyo ni biashara au ni huduma kwenye masuala ya VAT? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kama Serikali tumeiona changamoto hiyo na tumeanza kuifanyia kazi. Niwaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba tunapokuja na sheria mpya jambo hili yawezekana
likawa limepatiwa ufumbuzi.
Mheshimiwa Spika, nia ya Serikali yetu ni kuhakikisha wananchi wetu wanapata huduma hasa za afya katika mrengo ulio mzuri na bila usumbufu wowote. Kwa hiyo, niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba jambo hili Serikali tumeliona na hasa hili la kodi ya VAT ambalo liko chini la Wizara ya Fedha na Mipango. Ahsante. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Niseme tu nasikitika kwa majibu ambayo ni rahisi, majibu mafupi, majibu ambayo hayaoneshi matumaini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri...
...anasema ubinafsishaji wa matawi 22 yaliyokuwa National Milling tumepata shilingi bilioni 7.4, ni masikitiko makubwa sana; na hii inaonyesha moja kwa moja kwamba sisi huu umasikini umetuandama. kwa sababu kama tunaweza tukatupa…
..ni masikitiko makubwa sana. Msheshimiwa Mwenyekiti, najenga hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna matawi kama Plot 33, Plot 5, Tangold yale matawi sasa hivi yote ni ma-godawn. Watu walionunua matawi ya National Milling ambayo yanafanya kazi ni Bakheresa na Mohamed Enterprises peke yake, lakini matawi mengine yote yaliyobaki yamekuwa ma-godawn na ninyi mnasema mnaenda kwenye viwanda, mimi hapa sijapata kuelewa. Nini hatima ya hayo mashirika ambayo sasa hivi ni ma- godawn badala ya kuwa viwanda? (Makofi)
(b) Kwanza niseme wazi kwamba na mimi ni mmoja kwenye taaluma hii ya usindikaji wa nafaka. Nimefanya kazi National Milling si chini ya miaka 10. Kwa upande wa Kurasini mnamo tarehe 31 Aprili, 2005 waliletewa barua aliyekuwa Meneja pale kwamba kiwanda hicho akabidhiwe Mohamed Enterprises anayekaribia kununua, alikabidhiwa tu kwa sababu anakaribia kununua. Si hivyo tu, wafanyakazi waliokuwepo pale mpaka leo hii wanaidai Serikali hii zaidi ya shilingi milioni 234.3, bado hatima yao haieleweki na kesi imekwisha. Vilevile si hivyo tu, tarehe 20…Hazina wameitwa mahakamani hawataki kwenda, nini hatima ya wafanyakazi wale?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza nini hatima ya hayo Mashirika ambayo yalikodishiwa na sasa sio viwanda ni ma- godown. Naomba kumkumbusha Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ilishaanza mchakato wa kufanya tathimini ya viwanda vyote vilivyouzwa na ambavyo vimegeuzwa matumizi.
Mheshimiwa Waziri wa Viwanda alishasimama hapa na kusema na ndiyo kauli ya Serikali, kwamba vyote hivyo vitarejeshwa Serikalini na vitaendelea kufanya kazi, na vitatafutiwa wawekezaji na wataendelea kuviendesha viwanda hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili linalohusu hatima ya wafanyakazi, ameshasema kesi iko mahakamani, ikishakuwa mahakamani naomba nisiliongelee hapa na ni imani yangu kwamba kesi hiyo itaendeshwa na itafika mwisho mzuri.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza niipongeze Serikali kwa uamuzi wa kufungua Benki ya Maendeleo ya Kilimo Mkoani Dodoma na kukubali kutoa mafunzo kwa wakulima wadogo wadogo Mkoani Dodoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo imeanzishwa kwa malengo ya kuwawezesha wakulima kupata mikopo kwa masharti nafuu na kwa haraka zaidi. Je, Serikali iko tayari kupunguza sasa riba ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo ili wakulima wengi wapate kufaidika? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo ni mkombozi kwa wakulima. Je, Serikali iko tayari sasa kuhakikisha kwamba mikoa yote wanapata matawi ya benki hii ili wakulima wasihangaike kwenda Dar es Salaam na Dodoma kufuatilia mikopo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Felister kwa kuwa mbele katika kufuatilia miradi ya maendeleo ndani ya Mkoa wetu wa Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ameuliza kuhusu kupunguza riba. Kwanza nimkumbushe kwamba Benki hii ya Maendeleo ya Kilimo ilianzishwa kwa malengo makuu mawili. Moja ni kuchangia utoshelezi na usalama endelevu wa chakula nchini na pia kusaidia mapinduzi ya kilimo kutoka katika kilimo cha kujikimu na kwenda kilimo cha kibiashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutimiza malengo haya, Benki ya Maendeleo ya Kilimo ili iweze kufanya kazi hizi ni lazima iwe na mtaji wa kutosha na pia imekuwa iki-lobby katika taasisi nyingine za kifedha ili ziweze kutoa mikopo katika sekta ya kilimo. Benki hii ili iweze kupata mtaji wa kutosha sasa hivi Serikali imeshairuhusu Benki ya Maendeleo ya Kilimo iweze kupata mkopo wa bei nafuu kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika na iko mbioni kuupata na nina uhakika itaweza kutoa mikopo hii kwa bei nafuu kwa wakulima wetu wadogo wadogo na wa kati.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, ili kutimiza pia malengo haya Benki yetu ya Kilimo iliandaa mpango wa biashara wa miaka mitano ambao umeanza kutekelezwa kuanzia mwaka 2017 - 2021. Katika kutekeleza mpango huu wa biashara wa Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo imedhamiria kufungua ofisi sita za kikanda ndani ya Tanzania, ambazo ni Kanda ya Kusini, Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Kati, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Kanda ya Ziwa Viktoria pamoja na Zanzibar. Baada ya kufunguliwa ofisi hizi za kanda nchi nzima ni imani yetu sasa tutaweza kuwafikia wakulima wetu kule walipo.
MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa mujibu wa Msajili wa Hazina, Benki ya Kilimo inawajibika kutoa huduma zake Tanzania nzima. Napenda kumuuliza Naibu Waziri, ni kwa nini benki hii haijafikisha huduma zake kule Visiwani Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la Msingi, katika utekelezaji wa mpango wa biashara wa Benki hii ya Maendeleo ya Kilimo, imepanga kufungua ofisi sita za kikanda na Zanzibar ikiwemo. Ni imani yangu baada ya kufungua Ofisi ya Kikanda Dodoma, Ofisi ya Kikanda ya pili itakayofunguliwa ni Ofisi yetu ya Visiwani Zanzibar.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha, nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa kuna miradi imeshaanza kutekelezwa, kwa mfano, Wilaya ya Mpwapwa tulikuwa na matarajio ya kujenga barabara za lami, Mpwapwa Mjini kilometa 10; na kwa kuwa fedha iliyoletwa ni kidogo sana na ni karibu Majimbo yote kuna viporo; je, fedha iliyobaki Serikali italeta fedha zote kwa Wilaya zote? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa fedha zinazotengwa kwa ajili ya kujenga Vituo vya Afya Mima na Mbori ni kidogo sana na ndiyo maana havijakamilika sasa zaidi ya miaka kumi; je, Serikali itaongeza fedha ili tukamilishe vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Lubeleje kwa jitihada zake za kufuatilia maendeleo ndani ya Mpwapwa na ndani ya Wilaya nzima ya Mpwapwa, wananchi wako wanakutegemea sana kaka yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ni kupelekwa fedha zote. Kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, upelekaji wa fedha hutegemea mapato ya Serikali na hivyo fedha hizi zinapopatikana, lengo la Serikali ni kuhakikisha bajeti yetu inatekelezeka kwa asilimia 100. Kwa hiyo, fedha hizi tutakapokuwa tumezipata fedha zote zitapelekwa na miradi yote tuliyopanga itatekelezwa kama ambavyo tulipitisha bajeti yetu.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili la Vituo vya Afya kuongeza bajeti, ni imani yangu Wizara ya Afya watakapoleta bajeti yao hapa tutaiona na tumelizingatia hilo, vituo vyote vya afya ambavyo vimejengwa miaka mingi havijakamilika tumevizingatia katika bajeti yetu ya mwaka huu 2017/2018.
MHE. ZAINAB MUSSA BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa mtu husajili namba kwa mujibu wa mahitaji yake na mahali alipo akiwa ni Tanzania Bara au Tanzania Zanzibar. Je, haiwezekani usajili huo kwa kuzingatia sayansi na teknolojia kuratibiwa pamoja?
Swali la pili, je, ni kitu gani kinachozuia mtu anayesajili namba zake Zanzibar kuweza kutumia namba hizo hizo akiwa Tanzania Bara kwa kuzingatia utaratibu uliowekwa?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi sheria hii siyo sheria ya Muungano na ndicho kitu kinachozuia namba za Tanzania Bara kutumika Tanzania Zanzibar na Tanzania Zanzibar kutumika Tanzania Bara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili tumeliona kama Serikali na Kamati kikao cha pamoja kinachoshughulikia kero za Muungano kimeliona na kikao cha mwisho kimefanyika tarehe 13 Januari, 2017 chini ya Uenyekiti wa Makamu wa Rais na kimetoa maelekezo kushughulikia kero zote za Muungano ikiwa ni pamoja na hii ya usajili wa magari. Hivyo, kwa Serikali yetu tumeliona na tunaona kwa sababu tumepewa maelekezo Mawaziri wa pande zote mbili, Waziri wa Fedha wa Zanzibar, Waziri wa Fedha wa Tanzania pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani, tutakaa pamoja kuhakikisha kero hii inaondoka, lakini kwa mujibu wa sheria itakapokuwa tayari sheria hii italetwa ndani ya Bunge lako Tukufu ili kama Bunge lako litaridhia, tuweze kubadilisha utaratibu huo.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri lakini napenda afahamu kwamba tunapozungumzia wazabuni tusisahau kwamba tunawazungumzia wafanyabiashara. Mara nyingi kama walivyosema wenzangu wafanyabiashara hawa wanapata pesa zao kutoka kwenye mabenki lakini maelezo yake anasema kwamba wale ambao hawajalipwa watalipwa pindi Serikali inapopata pesa. Napenda kujua ni lini? Ni vizuri jambo hili sasa likawekewa mkakati.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu inatambua umuhimu wa kuwalipa wazabuni hawa lakini kama alivyosema Mheshimwa Naibu Waziri wa TAMISEMI kwamba sasa hivi tuliji-engage kwenye kuyahakiki madeni haya. Waheshimiwa Wabunge, naomba niwaambie jambo moja kwamba Serikali ina nia njema. Tulipokea madeni haya kwa ajili ya shule tu ya shilingi bilioni 21.64 baada ya uhakiki tumekuta ni shilingi bilioni sita tu ambazo ni halali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ndiyo maana Serikali inaomba muda maalum ili tuweze kumalizia uhakiki. Hii itasaidia Serikali kulipa yale madeni ambayo ni halali kwa ajili ya wazabuni waliotoa huduma na siyo kuwahi kulipa wakati kuna vitu vingine vya kufanya na tutajikuta tunalipa madeni hewa. Tunasisitiza dhamira ya Serikali ni njema na tutalipa madeni yote yale ambayo ni halali tu.
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia wafanyabiashara nchini iliweza kuahidi kugawa hizi mashine bure ili kurahisisha ufanyaji wa hii miamala. Je, zoezi hili limefanyika kwa kiwango gani na Serikali ina mpango gani wa kukamilisha?(Makofi)
Swali la pili dogo, sasa hivi tunafanya miamala kielektroniki kwa mfano kulipa gharama mbalimbali kama vile umeme, muda wa maongezi wa simu, ving’amuzi, kupitia kampuni za simu. Serikali itakubaliana na maelezo ya wafanyabiashara wanaoandaa mahesabu kwamba tulifanya malipo hayo kwa njia ya kimiamala?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa swali lake la kwanza ni kweli Serikali iliahidi kugawa mashine hizi na kwa sasa tumefikia hatua nzuri, maana yake tulisitisha zoezi ili tufanye tathmini ya zile mashine tulizozigawa ili sasa kuweza kugundua changamoto na fursa nyingine katika utekelezaji wa suala hili na uthamini huu unakaribia kukamilika na muda siyo mrefu tutaendelea kuzigawa mashine hizi kwa wafanyabiashara wote ambao wako registered kwa ajili ya VAT.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu malipo ya kielektroniki ni sahihi yanafanyika katika miamala ya simu kulipia malipo mbalimbali na sisi tunashirikiana na tayari tumeisha saini Memorandum of Understanding at TCRA ili malipo yote yanayofanyika kupitia simu au e-payment yoyote ile tuweze kui-truck na kuhakikisha document zote na kumbukumbu zote zinaweza kupatikana kwa ajili ya kufanya uthamini kwa ajili ya kodi. (Makofi)
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wadogowadogo
wa miti ambayo inazalisha mbao na kuni wa Mkoa wa Njombe na maeneo mengine ya Mkoa wa Iringa wamekuwa wakipata usumbufu mkubwa sana wanapovuna mbao zao na kutaka kupeleka sokoni. Wakifika Iringa wanakutana na kodi nyingine au wanakutana na utaratibu mwingine kwamba lazima wawe na risiti za EFD wakati hao wakulima wamevuna mazao haya kwenye shamba lao, na wamepata kibali cha kuvuna na kodi nyingine wameishatoa, lakini wanaambiwa wawe na risiti ya EFD na hawana mashine. Wasipokuwa na risiti ya EFD wanaambiwa watoe faini ya shilingi milioni moja. (Makofi)
Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu mzuri wa kuweza kuondoa hii kero ambayo imekuwa tatizo kubwa sana kwa wakulima wetu hususani wa Lupembe na maeneo mengine wanaosafirisha mbao zao kwenda sokoni Dar es Salaam? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi na Mheshimiwa Mbunge kama atakumbuka nimekaa naye kujadili tatizo hili na tayari nimeshaelekeza Mamlaka ya Mapato Tanzania kufuatilia jambo hili, ni risiti za aina gani zinazodaiwa Iringa tu.
Kwa hiyo, naahidi kwamba hili linafanyiwa kazi, nami nilimuahidi Mheshimiwa Mbunge nikimaliza kipindi hiki cha bajeti nitakwenda Iringa kushughulikia tatizo hili. (Makofi)
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba EFD ni mashine ya kukusanya kodi na kutoa risiti, kwa maana nyingine ni device ya TRA ya kukusanyia kodi, sasa kwa nini Serikali isiwape wafanyabiashara EFD mashine bure?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, EFD ni sahihi ni kwa ajili ya matumizi ya kikodi pia kwa matumizi ya wafanyabiashara wetu ili waweze kujua kumbukumbu sahihi katika kufanya biashara zao. Katika hili ndiyo maana Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kwamba EFD zigawiwe bure, lakini tuangalie mfumo mzuri wa kuweza ku-share gharama hizi za kupata mashine hizi za EFD. Kwa hiyo, Serikali inawekeza lakini na wafanyabiashara wetu nao wanawekeza kwa pamoja ili tuweze kujenga Taifa letu.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, naomba kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Kwa kuwa Serikali imejidhatiti kukusanya mapato kwa kupitia mashine hizi za EFD, lakini kuna matatizo makubwa ya kutokuwepo kwa mtandao au mawasiliano tunapoenda kwenye vituo vya manunuzi, vinavyosababisha wanunuzi kukaa kwenye vituo kwa muda mrefu wakisubiri risiti au wakati mwingine tunakata tamaa tunaondoka bila kuwepo na risiti.
Je, Serikali ina mpango gani makini kuhakikisha kwamba inaboresha mfumo wa kukusanya kodi pamoja na kupata huduma kwa muda unaotakiwa ili kuhakikisha kwamba kile walichokikusudia kinaliletea Taifa mapato kwa maendeleo yetu? Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakiri kwamba lipo hili tatizo kwa baadhi ya wauzaji na wafanyabiashara ndani ya nchi yetu. Tatizo la kimtandao halipo kwa kiwango ambacho wafanyabiashara wanakisema, nitoe wito kwa Wabunge kama viongozi kwenye maeneo yetu tushikamane na Serikali yetu kwa sababu hakuna maendeleo bila kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tushirikiane katika kuhakikisha wafanyabiashara wanatumia mashine hizi kwa pamoja, lakini TRA wanafanya jitihada kubwa za kupita maeneo ya wafanyabiashara wetu kuhakikisha kwamba mashine hizi zinatumika na zinafanya kazi. Ni wito wangu kwenu Waheshimiwa Wabunge tushirikiane kuhakikisha hili linaweza kufanyika ndani ya nchi yetu.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante,kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwa kuwa Serikali imekuwa ikihaidi kwamba itarejesha kodi hii ya majengo kwenye halmashauri zetu na ni ukweli kwamba mmekuwa hamrudishi; kwa mfano Halmashauri ya Kinondoni kabla haijagawanyika mliahidi mtarejesha bilioni 10 ikiwa ni sehemu ya makisio ya halmashauri husika, lakini mpaka leo hamjarudisha; je, Serikali hamwoni kwamba jambo hili hamliwezi sasa mtamke rasmi kwamba mtabakiwa na hizo kodi? (Makofi)
Mheshiiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano katika kila mwaka wa fedha imekuwa ikiendelea kuzinyang’anya halmashauri zetu vyanzo vingi vya mapato kiasi kwamba halmashauri nyingi sasa hivi zinaelekea kushindwa kujiendesha kwa sababu Serikali Kuu inachukua fedha zote; je, Serikali haioni umuhimu sasa mlete mabadiliko ya Katiba hapa Bungeni mzifute rasmi Serikali za Mitaa?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa si kwamba hatuwezi jambo hili, hilo nakanusha. Nimesema hapa ufanisi halisi tukilinganisha kati ya halmashauri pamoja na TRA. Katika hili naomba nilieleze Bunge lako Tukufu kwamba sote sisi ni Watanzania na zote tumeona tarehe za mwisho wa mwezi wa Sita wananchi walivyotoka kwa wingi kwenda kulipia kodi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kusema Serikali tumeshindwa si sahihi kabisa na ndiyo maana Serikali kwa kuangalia wananchi wetu jinsi ambavyo wamelipokea jambo hili kwa matokeo mazuri kabisa tumeongeza wiki mbili na naomba mtupime Serikali baada ya hizi wiki mbili ni ambacho tutakuwa tumekifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la kubadilisha Katiba ya Nchi naomba nimwambie Mheshimiwa Cecilia kwamba kwenye jibu langu la msingi nimesema kwamba mamlaka yenye mamlaka halisi ya kukusanya mapato ya nchi yetu ni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na ndicho ambacho kwa mujibu wa Sheria Mheshimiwa Waziri wa Fedha amekifanya na tunaendelea kufanya hatujafanya kitu chochote ambacho kiko kinyume na katiba kinachotupelekea kuleta Mabadiliko ya katika Katiba katika Bunge lako. (Makofi)
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la msingi lilikuwa linauliza kiasi cha Deni la Taifa hadi sasa. Mheshimiwa Waziri hakujibu kabisa hilo ndiyo swali limeulizwa lakini hakulijibu hilo kabisa! Amekuja na mambo mengine mengi tu.
Kwa kuwa yote aliyosema Mheshimiwa Waziri katika kujibu swali hili ameonesha kwamba mwaka huu wa fedha 2017/2018 Serikali imejipanga kukopa shilingi trilioni 8.83 ambapo wastani kwa mwezi ni sawa na kukopa shilingi bilioni 652 na mishahara ni takribani shilingi bilioni 600. Kwa hivyo kwa mwezi tutakuwa tunalipa mishahara pamoja na kulipa Deni la Taifa. Je, fedha za maendeleo zitapatikana wapi kama tutakuwa tunalipia tu Deni la Taifa pamoja na mishahara?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Serikali ya Awamu ya Tano ilivyoingia madarakani Deni la Taifa lilikuwa ni shilingi trilioni 35 lakini hadi mwezi Machi mwaka huu deni la Taifa limeongezeka na kufika shilingi trilioni 50.8 kwa kasi kubwa namna hii ya kukopa tunalipeleka wapi Taifa letu ambapo tutaweza tukaangamia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa James Mbatia kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda kuliambia Bunge lako tukufu swali kama lilivyoulizwa ndivyo nilivyolijibu kwa sababu limeulizwa tangu tumepitisha Mpango wa Maendeleo. Mpango wa Maendeleo tunaoutekeleza sasa ni mpango tulioupitisha mwaka 2016/ 2017 na ndio tunaoutekeleza na ndivyo tulivyojibu swali letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upatikanaji wa fedha za maendeleo; upatikanaji wa fedha za maendeleo unapatikana kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba tunaimarisha ukusanyaji wa mapato, kwa hiyo, tunaweza kulipa deni letu na deni letu la ndani inakuwa ni rollover.
Kwa hiyo, hiki alichokisema Mheshimiwa James Mbatia inawezekana kabisa kwa sababu hii ni rollover tuna roll mikopo yetu tunaweza kulipa riba yetu na tunaweza kulipa deni letu la nje. Kwa hiyo, tuna uwezo wa kulipa deni letu na tuna uwezo wa kuendelea kutekeleza miradi yetu ya maendeleo kama tulivyofanya mwaka huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ameuliza tunalipeleka wapi Taifa letu. Napenda kurejea kauli yangu niliyoisema ndani ya Bunge lako Tukufu kwamba what matters is not how much you have borrowed but for what have you borrowed; tunakopa ili kutekeleza miradi ya maendeleo, miradi ya kimkakati, miradi inayochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa letu na hakuna duniani hata Marekani yenyewe inakopa na inaweza kutekeleza miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunachokiangalia uchumi wa Taifa letu unakuwaje, miundombinu ya Taifa letu inayopelekea ukuaji wa uchumi wetu inatekelezwa kwa kiasi gani. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. KHAMIS MTUMWA ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa taasisi hizi za Ubalozi ni taasisi za Muungano je, haoni ipo haja sasa ya kushirikiana na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Zanzibar katika kukagua taasisi hizo?
Pili, kwa kuwa tuna mahusiano mazuri katika taasisi hizi za Muungano, yeye Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba hajaona ulazima; je, haoni sasa imefika wakati wa kushirikiana na kuonesha Muungano wetu huu unadumu na kuondosha kero ndogo ndogo ambazo zinatokezea kama hizi za kutokushirikishana? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nia ya Serikali yetu na lengo lake kwa Muungano ni kuudumisha Muungano wetu katika kila nyanja, kama alivyosema Mheshimiwa Rais wetu katika sherehe za Muungano za mwaka huu 2017 kwamba Serikali yetu inaupenda Muungano na tutaulinda kwa ngazi zote na nguvu zote, hiyo itabaki hivyo. (Makofi).
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema mwanzo jukumu hili la ukaguzi ni la Kikatiba na Kisheria. Ofisi zote za Muungano hukaguliwa na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini akiona inafaa Mkaguzi huyu anaweza kumshirikisha Mkaguzi yule. Tuelewe tu kwamba kikatiba na kisheria siyo lazima, lakini kimahusiano anaweza akafanya hivyo. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS,
(MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuongezea katika majibu mazuri kabisa yaliyotolewa na Naibu Waziri wa Fedha, kwamba pamoja na mgawanyo wa majukumu ya kikatiba na kisheria kuhusu mamlaka za ukaguzi maeneo na taasisi zinazopaswa kukaguliwa, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wakaguzi hawa na Wadhibiti Wakuu wa Serikali zote mbili wanashirikiana kwa karibu sana katika kubadilishana uzoefu, pia kujenga uwezo wa kitaasisi hasa kwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa upande wa Zanzibar. Hilo ndilo ambalo tunalihimiza na tunalisisitiza lamahusiano na ushirikiano wa taasisi za pande zote mbili hata katika masuala ambayo siyo ya Muungano.(Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Serikali imekuwa ikidaiwa fedha nyingi sana na mifuko ya hifadhi, mfano, PSPF ilikuwa inaidai Serikali zaidi ya shilingi 2,671,000,000,000 pia LAPF ilikuwa inaidai Serikali zaidi ya shilingi bilioni 47 kwa ajili ya asilimia 15 ya makato kwa ajili ya wafanyakazi. Je, Serikali imelipa kiasi gani na hali ikoje kwa wastaafu hawa mpaka sasa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa Serikali ilikuwa ikidaiwa kama hiyo asilimia 15, shilingi trilioni 1.4 mpaka sasa tumeshalipa trilioni 1.1, bado shilingi bilioni tatu, ambayo mwezi huu Mei, tunakamilisha kulipa hiyo iliyobaki. (Makofi)
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitegemea majibu ya Serikali yaende mbali zaidi, kwamba mbali ya kuelezea huu utaratibu lakini ijiridhishe kama kweli huo utaratibu unafuatwa. Wastaafu wa Zanzibar wamekuwa wakilipwa kwa mikupuo mitatu, maana yake ni miezi minne badala ya miezi mitatu, mitatu kama utaratibu unavyosema.
Je, ni lini Serikali itaanza kuwalipa kwa miezi mitatu badala ya miezi minne kama utaratibu unataka?
Swali la pili, Bunge la Kumi lilipandisha viwango vya pensheni vya kima cha chini kutoka shilingi 50,000 kwenda shilingi 100,000, mpaka leo baadhi wastaafu hawa baadhi ya wastaafu hawajawahi kulipwa hicho kiwango kipya. Tuliwahi kuuliza hapa na Naibu Waziri wa Fedha akasema kwamba kufika Februari, 2016 wangeanza kulipwa viwango hivyo vipya pamoja na arreas zao. Nataka kujua kwa wale wastaafu wote ambao hawalipwi kupitia Hazina ni lini wataanza kulipwa viwango vipya vya shilingi 100,000?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la kwanza kwamba wastaafu wa Zanzibar wanalipwa miezi minne, minne, napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba hata wastaafu wa Bara waliokuwa wakilipwa na Hazina walikuwa wakilipwa miezi mitatu mitatu na sasa hivi kuanzia Oktoba 2016, wanalipwa mwezi mmoja, mmoja na tulipokuwa tunafanya uhakiki wa wastaafu wetu, zoezi ambalo linaendeshwa na Wizara ya Fedha tumekuwa tukikusanya mawazo yao kwamba nini wanapendelea na tutakapokuwa tumekamilisha utafiti huo tutakaa chini na kuweza kutoa maelekezo ya Serikali kwamba watalipwaje. Hivyo, hii inakwenda kwa wastaafu wa Zanzibar kwamba na wao tutachukua maoni yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kusema kwamba Serikali imekuwa ikifuata sheria katika kulipa mafao haya, lakini pia kuweza kuchukua mawazo ya wastaafu hawa kwa sababu wao ndiyo wafaidika. Kwa mfano, hii ya sasa hivi hii ya kwenda mwezi mmoja, mmoja kwa wastaafu wa Bara wamekuwa wakilalamika kwamba ile miezi mitatu, mitatu japo kuwa ni wao ndiyo walipendekeza na sheria yetu ikaruhusu lakini wanalalamika kwamba wanakosa kupata mikopo kwa sababu cash flow haiko vizuri. Serikali imewasikiliza na kuanza kulipa mwezi mmoja mmoja na hao wa Zanzibar pia tutasikiliza tutaangalia na sheria zetu wataweza kulipwa kwa vile ambavyo wao wanapendelea na sheria yetu inaruhusu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swalli la nyongeza ya shilingi 50,000 nakumbuka nilijibu hapa katika hapa katika Bunge lako Tukufu, kwamba wale wastaafu wote wanaolipwa na Hazina nyongeza yao walianza kulipwa na wote wanalipwa shilingi 100,000 kwa sasa. Kwa wale wanaolipwa na mifuko nililiambia Bunge lako Tukufu kwamba baada ya kutolewa agizo lile la Serikali, Bodi ya Wakurugenzi wa Mifuko husika, walitakiwa kukaa na kuweza kukubaliana ni lini wanaanza kulipa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niwaambie wastaafu wote nchini, kwamba hii tuliyoisema shilingi 50,000 kwenda shilingi100,000, moja kwa moja ilikuwa ni wale wastaafu wanaolipwa na Hazina. Wale wa mifuko, Bodi zao za Wakurugenzi watafanya tathmini na wataanza kuwalipa kama ambavyo mfuko wetu wa PPF wameshafanya tathmini na sasa tangu Januari 2017, wameanza kulipa shilingi 100,000 kwa wastaafu wote wa kima cha chini.(Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANAM AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba kwanza niwapongeze Naibu Mawaziri wote wawili kwa majibu mazuri ya nyongeza.
Naomba niongeze jambo moja tu dogo nilialifu Bunge lako Tukurfu kwamba SSRA wameshamaliza kufanya tathmini ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii yote katika nchi yetu ya Tanzania pamoja na PPF kuanza kulipa kima cha chini cha pensheni cha shilingi 100,000 pia Mfuko wa NSSF na LAPF wameshakamilisha tathmni hiyo na wao wameshaanza kuendelea na mchakato huo wa kupandisha kima cha chini. Kwa hiyo, Serikali imeshatekeleza agizo hilo kwa kiasi kikubwa na utekelezaji wa malipo hayo sasa umeanza kufanyika hata kwenye Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii.
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa mikopo isiyolipika (non performing loans) imekuwa kwa kikubwa sana tangu miaka 1990, na sababu kubwa ni mbili, ya kwanza ni mazingira magumu ya biashara na ya pili ni riba kuwa juu.
Swali, ni kwanini, Serikali haioni haja ya kuwasaidia wafanyabiashara kwa kuwapa riba yenye mikopo nafuu kama njia ya stimulus package?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa muda mrefu Serikali yetu imekuwa ikijinadi kuwa yenyewe ni Serikali ya Kijamaa, na misingi na Sera ya Serikali ya Kijamaa ni pamoja na kuwa ukomo wa riba. Je, ni lini Serikali itaweka ukomo wa riba kama ambavyo nchi ya kibepari ya Kenya imeweka ukomo wa riba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, kutokana na mfumo wa mwaka 1991 na Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha, Benki Kuu au Serikali haiwezi kutoa mwelekeo au ukomo wa riba kwa ajili ya benki na taasisi za kifedha. Nchi yetu ni nchi huru inayofuata liberalization of the economy na hilo haliwezi kufanyika kwa sababu nimesema ni sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, nchi ya Kenya iliweka ukomo huo lakini imeingia katika matatizo makubwa ya kiuchumi kwa benki na taasisi za kifedha. Hivyo nchi yetu kama nchi huru inayofuata liberalization of the economy hatuwezi kufanya hivyo kwa sababu ni sheria iliyopanga hivyo.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niulize swali dogo la nyongeza.
Serikali ina mpango gani wa kulipa fidia kupitia Wizara mbalimbali ikiwemo Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji juu ya wajasiriamali wakiwemo wa Makambako juu ya Soko la Kimataifa, nini kauli ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Serikali ilitoa kauli wakati tunapitisha bajeti ya Wizara ya Ulinzi na kuhusu wafanyabiashara wajasiriamali wa soko la Makambako naomba kumwambia Mheshimiwa Sanga kwamba Serikali sasa inafanya uhakiki wa mwisho, itakapokuwa imekamilisha kufanya uhakiki huo Serikali itaanza kuwalipa wajasiriamali na wananchi wote ambao wanastahili kulipwa fidia katika maeneo mbalimbali yaliyotwaliwa na Serikali.
MHE. KABWE Z. R. ZITTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2016 mikopo ya benki kwenda kwenye sekta binafsi imeporomoko kuliko wakati mwingine wowote katika kipindi cha miaka ishirini iliyopita.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Fedha inachukua hatua gani madhubuti ya kuhakikisha kwamba wajasiliamali na hasa viwanda na wafanyabiashara wanaendelea kupata mikopo benki kwa kuboresha hali ya uchumi wa nchi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba hali ya uchumi wa Taifa letu bado iko imara na iko vizuri na si kwamba kutokupewa mikopo kwa sekta binafsi kunaashiria kuporomoka kwa uchumi, hilo naomba niliweke vizuri hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimwambie kwamba Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango na Benki Kuu imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuhakikisha mikopo hii kwa sekta binafsi inaendelea kutolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba, benki zetu zimekaa vizuri sasa katika kuhakikisha zinadhibiti mikopo chechefu ambayo imekuwa ikizisumbua miaka mingi iliyopika. Kwa hiyo ni usimamizi madhubuti uliowekwa na Benki Kuu kupitia Wizara ya Fedha na Mipango, na tunaendelea kusimamia kuhakikisha kwamba kabla ya benki na taasisi za kifedha hazijatoa mikopo wahakikishe mtu wanaempa mikopo ni nani na ana uhakika gani wa kurejesha mikopo ambayo ipo.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na riba kubwa inayotozwa kwa wafanyabiashara wadogo lakini pia wafanyabiashara wadogo wanachangamoto kubwa ya tozo za ada na ushuru katika makundi haya ya bodaboda, mama ntilie na wauza mbogamboga. Na kwa kuwa Serikali yetu kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi iliahidi Itazitazama upya tozo hizi ambazo ni kikwazo kwa wafanyabiashara wadogo, sasa ni lini Serikali yetu itatazama upya tozo hizi ili wafanyabiashara wadogo waweze kupunguziwa mzigo mkubwa katika uendeshaji wa biashara yao?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Bunge lako Tukufu limeona kupitia Wizara ya Kilimo kuna tozo ambazo zimependekezwa nyingi tu kuondolewa, ambazo serikali iliahidi kuziondoa. Na nyingine ambazo haziko chini ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali iko kwenye mchakato wa kuandaa Tax Measures na Finance Act, 2017, hivyo tuvute subra, yote haya ambayo Serikali yetu iliahidi yote yatatekelezwa.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza, lakini sambamba na hiyo nakushukuru sana kwa kuweza kunipa pongezi kwa swali langu la ki-CPA. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri amejibu vizuri, lakini kodi hii inasema ni road licence na yeye anasema ni kodi ya usajili wa gari ya mwaka kwa hiyo ni vitu viwili tofauti. Kwa hiyo, napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri, je, haoni kwamba kodi hii kwanza inakusanywa kimakosa kwa sababu jina leke liko tofauti na lilivyo na pili haoni kwamba ingekuwa bora zaidi tungeikusanya kwa kutumia matumizi ya gari barabarani ili kuongeza kama mapato yake?? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kuna baadhi ya watu sasa wanasumbuliwa barabarani, kwa kudaiwa madeni ya gari ambayo pengine ina muda mrefu haifanyi kazi ipo nyumbani na wanadaiwa kwamba lazima alipe kodi hiyo. Je, Mheshimiwa Waziri haoni kwamba kuna haja ya kutoa tamkoili watu wasisumbuliwe barabarani na traffic, polisi, pamoja na TRA juu ya suala hili la kulipa kodi hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kiutaalamu kodi hii au ada hii haitwi road licence, kama Sheria inavyosomeka pamoja na kanuni zake, zinasomeka The Road Traffic Motor Vehicles Registration, kwa hiyo hii ni motor vehicle ni ownership kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi. Sio kwamba inalipiwa kwa matumizi yake barabarani, kwa hiyo, sheria inasema hivi, lakini kwa lugha zetu za mtaani tunaiita hivyo. Lakini kimsingi hii ni ownership na sio sheria ya kutumia ni ada ya kutumia gari barabarani, hapana.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, ada hii ya leseni ya gari ya mwaka hutozwa kwa kila gari kulingana na ukubwa wa engine ya gari na kwa sasa kwa jinsi ilivyo sheria hii haitoi fursa ya kusamehe ada hii ambayo haikulipwa huko nyuma.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba ipo katika kanuni zetu sehemu ya nane kifungu cha 32 mpaka 34 inamuelekeza owner wa vyombo vya moto jinsi ya kufanya utaratibu upi afuate kama chombo chake hakitumii tena, haki-own tena ili aweze kwenda kwa registrar ambaye ni Katibu Mkuu Hazina ili aweze sasa chombo chake kuwa deregister na hataweza kudaiwa tena ada hiyo.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema hii ni sheria lakini kama Serikali tumesikia kilio cha Wabunge wengi pamoja na wananchi tunalifanyia kazi, tunaifanyia kazi sheria pamoja na kanuni zake kuona jambo hili linafika mwisho ambao ni mzuri kwa Serikali yetu pamoja na wananchi wetu.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, kumekuwa na malalamiko mengi sana, hii inaitwa road licence kama anavyosema, gari yangu mfano imekaa jikoni, uani, garage miaka mitatu, sina pesa za kutengeneza lakini nikadaiwa hiyo road licence na faini juu. Kwa nini Serikali isione kwa sasa kwamba kwa nini wasiingize kwenye mafuta ili gari yangu ikitembea mimi nilipie kodi moja kwa moja kuliko kumtesa mtu gari yake imekaa jikoni miaka mitatu aendelee kulipa kodi wakati hana uwezo hata kununua spare. Gari yake kama anavyosema imepata ajali, lakini gari inaweza kukaa miaka mitatu, asiyekuwa na uwezo wa kutafuta pesa, lakini itaendelea kudaiwa road licence na inapigwa na faini juu, hii ni halali kweli? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa nini msichukue kigezo cha kuweka kwenye mafuta, pesa kwenye mafuta, ili ninapotembeza ile gari yangu nalipia moja kwa moja road licence?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, najua ni jambo muhimu sana hili kwa Taifa letu na kwa wananchi wetu. Kama Serikali tumesikia na tunalifanyia kazi kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya mwanzo, lakini naendelea kusisitiza na kumwambia ndugu yangu Ally Keissy hii tunalipia umiliki na sio matumizi ya gari yako barabarani.
MHE. RASHID M. CHUACHUA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba niulize swali moja la nyongeza. Ni kweli kuwa si kila msamaha wa kodi una madhara katika jamii na uchumi, hata hivyo ipo misamaha ya kodi isiyo na tija. Kwa kuwa hadi kufikia mwaka 2015/2016 misamaha ya kodi ilifikia asilimia 8.6 ya mapato yote ya kodi. Mpango wa Serikali ni upi kuhusu misamaha ya kodi kwa mwaka wa fedha 2017/2018? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ameuliza mpango wa Serikali kwa mwaka huu. Naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali sasa hivi iko katika mchakato wa kuangalia tax measures itakayohusishwa na misamaha ya kodi kwa mwaka huu. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge awe na subira, tarehe nane ni keshokutwa, Serikali yetu italeta mapendekezo yote na Bunge lako Tukufu litapitisha hayo mapendekezo ya Serikali. (Makofi)
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, imekuwa ni mazoea ripoti kadhaa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika miaka mbalimbali zimekuwa zikionyesha kwamba mafao ya wastaafu yanakuwa yakipunjwa kwa makusudi na Serikali imekuwa ikieleza kwamba ni wakati wa kukokotoa ndiyo matatizo hayo yanatokea.
Je, ni kwa nini basi mmekuwa mkiwapunja na kuwanyanyasa kwa makusudi na hali zao za maisha zimekuwa ni mbaya na tatizo hili limekuwa la muda mrefu, CAG analalamika lakini Serikali imekuwa haifuatilii kwa makini, tabia hii mbaya ya Serikali ya kuwapunja/kuwadhulumu wastaafu mtaacha lini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ni kwamba shilingi 50,000 ambayo ilikuwa miaka iliyopita mkapandisha mpaka shilingi 100,000 ambayo ni wastani wa shilingi 3,300 kwa siku. Katika majibu yako ukasema kwamba sasa mnajielekeza kwenye miundombinu ya usafiri, usafirishaji, nishati na umeme, hivi watu hawa ambao mliwatuma wakiwa wazima wakafanya kazi hii kwa uadilifu na uaminifu mkubwa mnawapatia shilingi 3,300, mtuambie waziwazi mkakati wa Serikali wa ziada wa kuboresha maisha ya wastaafu kwa kuongeza pensheni hii utafanyika lini siyo kubakia na majibu haya tu kwamba mnajielekeza kwenye usafirishaji na usafiri hawa mnawatuma wakiwa na nguvu sasa mmewaacha mnawatelekeza, tabia hiyo mbaya Serikali mtaacha lini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa swali lake la kwanza, kusema kwamba Serikali ina tabia mbaya ya kuendelea kuwapunja wastaafu wetu, hii siyo sahihi hata kidogo. Nasema siyo sahihi hata kidogo kwa sababu nimemueleza mafao ya wastaafu hukokotolewa kwa kanuni ambayo imekubalika ndani ya Serikali na wastaafu, kwa hiyo, hakuna sehemu yoyote ambako mstaafu anapunjwa na Serikali yetu, hilo halipo hata kidogo. Kwa hiyo, kanuni iko wazi na inatumika na kila mstaafu anapojiunga na mfuko wowote huiona kanuni hii kabla ya kujiunga na mifuko hii.
Kwa hiyo, napenda wananchi wetu waelewe, Serikali yetu ina nia njema na dhamira ya dhati ya kuhakikisha wastaafu wanalipwa katika msingi ambao ni mzuri kabisa na ndicho ambacho Serikali tumekuwa tukifanya. Ndio maana 2015 tumeongeza kiwango hiki kutoka shilingi 50,000 mpaka shilingi 100,000 kima cha chini. Wapo wanaolipwa vizuri zaidi kwa sababu nimesema formula hii inategemea na muda wake wa utumishi pamoja na mshahara wake wa mwisho aliostaafu nao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili kwamba Serikali ina mkakati gani, nimemueleza vizuri kabisa kwamba Serikali yetu na sote sisi ni mashahidi tunapambana kuhakikisha tunaongeza mapato ya Taifa letu, tunaweza kukusanya kodi yetu na sote tunaona.
Pia nimesema wazi, ukiongeza pensheni kwa ajili ya wastaafu tu wakati hakuna dawa, maji na huduma nyingine muhimu za jamii haitoleta maana yoyote kwa Taifa letu. Tunawathamini wastaafu wetu, tunaendelea kufanya nao kazi vizuri na tutaendelea kuwalipa jinsi ambavyo mapato ya Taifa letu yanavyoimarika.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ni kweli kabisa kwamba wastaafu wanateseka sana na wengi wao wanapoteza maisha. Ni katika Bunge hili hili, Mheshimiwa Naibu Waziri aliliahidi Bunge kwamba wastaafu wote wanaodai malimbikizo baada ya marekebisho ya kima cha chini kutoka shilingi 50,000 kwenda shilingi 100,000 watalipwa fedha zao kwa maana arrears zote lakini ni takribani miaka miwili sasa wastaafu hawa hawajalipwa fedha zao sana sana ni wale ambao walikuwa kwenye PSPF na PPF.
Mheshimiwa Naibu Spika, ningetaka kujua ni kwa nini Serikali haijaweza kuwalipa hawa wastaafu haya malimbikizo kama ambavyo Naibu Waziri uliahidi Bunge hili na je mnavyoenda kuwalipa…
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kukanusha kwamba ni miaka miwili wastaafu hawa hawajalipwa ile nyongeza, siyo sahihi hata kidogo. Mifuko yote ya Hifadhi ya Jamii wameanza kulipa kima cha chini kilichoongezwa na Serikali kuanzia mwezi Januari, 2017. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hili aliloli-quote yeye kwamba niliahidi hapa, nakumbuka wakati najibu swali hili nililieleza Bunge lako Tukufu kwamba kulingana na Sheria ya SSRA, regulator anaye-regulate Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii, ni Bodi za Wadhamini za mifuko husika baada ya actuarial valuation ndizo zinazoamua sasa kulipa kiwango hiki na ndipo baada ya kufanya actuarial valuation Bodi zote zimeidhinisha na tumeanza kulipa kwa kipindi chote kuanzia Januari mpaka leo tunapoongea wote wanalipwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, najua yapo malalamiko wanasema kwamba wengine hawaoni hizo transaction lakini naomba niwaambie kwamba hasa kwa wastaafu wetu wanaolipwa na PSPF siku za nyuma pensheni zao za kila mwezi zilikuwa zikianza kulipwa kabla ya hii addition kwa hiyo kulikuwa kunaonekana kuna two transaction ndani ya mwezi mmoja kwa utofauti wa wiki moja au wiki mbili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali yetu inalipa nyongeza hii kwa sababu nyongeza hii hasa kwa PSPF hulipwa kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina, tunalipa kwa wakati na wanalipwa siku moja pensheni yao pamoja na ile nyongeza yao. Kwa hiyo, hakuna sehemu yoyote ambapo hawalipwi.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa, mpaka sasa hivi kuna baadhi ya makampuni ya watu binafsi na wafanyabiashara wanaendelea kutoza na kupanga bei kwa kutumia dola badala ya Tanzanian shillings.
Je, Serikali haioni hiyo inaidhalilisha shilingi yetu na kuonesha kwamba, hawana imani na shilingi ya Tanzania?
Swali la pili, kwa kuwa moja ya eneo ambalo linatumia fedha nyingi sana na kusababisha kutokuwepo kwa urari mzuri wa nchi ni uagizaji wa vyakula mbalimbali kutoka nje ya nchi wakati vyakula hivyo vinaweza kuzalishwa ndani ya nchi, maeneo kama mafuta ya kula, sukari na mazao mengine ambayo yanaweza kuzalishwa hapa nchini. Kwa mwaka tunatumia zaidi ya shilingi trilioni 2.8 kwa ajili ya kuagiza mazao yanayotokana na vyakula vinavyoweza kuzalishwa hapa na kutoa ajira kwa wananchi.
Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuzuia uagizaji wa baadhi ya vyakula kutoka nje ya nchi ili kuinua ualishaji wa ndani ya nchi na kuokoa shilingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza kwamba katika watu ambao wanaweka bei kwa kutumia dola wanaidhalilisha shilingi yetu, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, tulipitisha sheria katika Bunge lako Tukufu kwamba siyo kosa kuweza kuweka bei kwa currency ambayo siyo ya Tanzania, kosa ni ni kukataa pesa shilingi ya Tanzania pale ambapo mteja anataka kulipa na yule mwenye duka akakataa kupokea hilo ndio kosa, lakini siyo kosa katika kuweka bei hiyo kwa currency ambayo sio shilingi yetu ya Tanzania, kama Taifa tuliona inafaa na ndiyo maana tunaendelea kutekeleza sheria hii tuliyopitisha mwaka 1992.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kuzuia ku-import bidhaa ambazo zinazalishwa hapa nchini. Napenda kulijibu Bunge lako Tukufu kwamba, ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tano inasisitiza kwamba uchumi wa viwanda ili tuweze kuzalisha bidhaa zetu za kutosheleza ndani ya nchi yetu. Tutakapokuwa tumeweza kuzalisha bidhaa hizi kwa kiwango ambacho kinatosheleza hatuna sababu ya kuendelea ku- import na tutaweza kurekebisha sheria zetu ili tuweze sasa kutumia bidhaa zetu, lakini kusema sasa tupige marufuku wakati bado kuna uhitaji wa bidhaa hizi, haitakuwa sahihi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuendelee kuiunga mkono Serikali yetu katika kuiendea Tanzania ya Viwanda, tuna uhakika ndani ya miaka mitano mpaka kumi tutakuwa tumeweza kujitosheleza kwa bidhaa zetu ndani ya Tanzania. (Makofi)
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kwa kinywa chake katika majibu yake ya msingi kwamba, kushuka au kupanda kwa thamani ya shilingi yetu hakuna uhusiano na utozaji wa bidhaa au huduma kwa dola.
Je, anataka kuwaaminisha wachumi wote Tanzania na duniani kote na Bunge hili kwamba hata miaka mitano tukiamua kutumia dola tu bila kutumia shilingi na baadaye tukairejea baada ya miaka mitano tutakuta uchumi wetu haujaathirika na wala shilingi yetu haijaathirika?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, si kuwaaminisha Wachumi, kama nilivyosema nimeeleza sababu ya kushuka kwa thamani ya currency yoyote ile hata kama sio shilingi ya Tanzania. Kuweka quotation kwa bei ambayo siyo shilingi ya Tanzania si sababu mahsusi, lakini naomba kumwambia Mheshimiwa Kangi Lugola kwamba ni asilimia 0.1 tu ya watu ambao wanaweka quotation kwa bei ambayo sio shilingi ya Tanzania ambao wako tayari kupokea fedha hii kwa kutumia currency ile waliyo-quote. Zaidi ya asilimia 99.9 ya Watanzania na wafanyabiashara wanaoweka quotation kwa pesa ambayo sio T-Shillings wako tayari kupokea bei yao na kuuza bidhaa zao na kupokea shilingi ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kangi Lugola kama nilivyosema ziko indicators. Viko viashiria mbalimbali vinavyosababisha kushuka kwa uchumi na hatuna sababu ya kusema kwamba tuweze kuweka miaka mitano tufanye quotation na tusitumie shilingi yetu ya Tanzania. Nimesema kupitia Sheria ya Benki Kuu ya mwaka 2006, Kifungu cha 26 ni shilingi ya Tanzania ndiyo legal tender document ambayo inaruhusiwa ndani ya Taifa letu. (Makofi)
MHE. HUSSEIN M. BASHE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninauliza swali moja la nyongeza.
Kutokana na ripoti ya BOT latest ya mwezi Juni, inaonesha kwamba export volume yetu imeshuka kutoka dola milioni 4.5 mpaka dola milioni 3.8 wakati huo huo prices za commodities kwenye soko la dunia imeendelea kushuka na import volume yetu ya capital goods imeendelea kushuka.
Je, Serikali ina mpango gani kutokana na variables hizi zote nilizozitaja kuhakikisha kwamba, miezi mitatu mpaka sita ijayo stability ya shilingi yetu inaendelea kuwa imara kwa sababu indications zote zinaonesha kwamba, shilingi yetu inaendelea kushuka kila siku kutokana na hali ya uchumi na uzalishaji?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa
Naibu Spika, kama ambavyo amesema ni kweli kwamba export volume yetu imeshuka, na mimi katika jibu langu la msingi nimesema katika miezi ambayo Taifa letu huwa linapanda katika exportation ni kuanzia Julai mpaka Disemba na ndio kipindi hiki. Kwa hiyo, nimuombe tu Mheshimiwa Bashe kwamba ndani ya kipindi hiki kwa sababu ndio tunazalisha na tunavuna export yetu itapanda muda siyo mrefu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimesema kwenye jibu langu la msingi kwamba tuendelee kuiunga dhamira ya Serikali yetu, Tanzania ya Viwanda ndiyo itakayotuwezesha kuongeza export volume yetu na kuweza kupunguza importation ya bidhaa ambazo tutazizalisha ndani ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuendelee kumuunga Mheshimiwa Rais wetu katika dhamira yake hii na sisi kama wasaidizi wake tuko imara katika kumsaidia kuhakikisha kwamba, thamani ya shilingi yetu inaendelea kuimarika na export volume kulingana na viwanda ambavyo tayari sasa vimeanza kufanya kazi, itaongezeka muda siyo mrefu. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini nilitaka nimpe Taarifa tu Mheshimiwa Hussein Bashe kwamba, katika record za hivi karibuni nchi yetu ina reserve nyingi na ina over five months of imports kutokana na credibility ya Government Policy. Kwa maana hiyo, kushuka kwa imports wala hakujaathiri sana matarajio ya kuharibika kwa ustahimilivu wa mfumuko wa bei kutokana na kwamba, Serikali ina reserve nyingi za kutosha na kwa maana hiyo export zitakapokuwa zimeongezeka zitakutana na reserve za kutosha ambazo hazitaleta uharibifu wowote kwenye mbadilishano wa fedha pamoja na mfumuko wa bei. (Makofi)
MHE. MATHAYO D. MATHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuuliza swali la nyongeza.
Aidha, napenda kumpongeza Naibu Waziri kwa kujibu maswali yake vizuri na kitaalam. Nina maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, Benki Kuu imepunguza riba ya mabenki ya biashara yanapokopa kutoka kwenye Benki Kuu hadi kufikia asilimia tisa na kwa kuwa pia, imepunguza amana kutoka asilimia kumi hadi asilimia nane ya kiwango cha fedha ambazo mabenki haya ya biashara yanatakiwa yahifadhi Benki Kuu. Je, Benki Kuu imefuatilia na kuona kwamba, mabenki ya biashara yanatoza riba nzuri au yametoa punguzo zuri la riba kwa wananchi ambao wanakopa kwenye mabenki hayo?
Swali la pili, kwa kuwa katika nchi zinazoendelea asilimia 70 ya fedha zinakuwa mikononi mwa wananchi na asilimia 30 inakuwa kwenye mabenki pamoja na Serikali. Je, Benki Kuu imefanya utafiti na kuona, kwa sababu sasa hivi tukiangalia fedha katika mzunguko kwa wananchi wa kawaida zimepungua sana.
Je, Benki Kuu imefanya utafiti na kujua kwamba, fedha hizi ziko wapi ili waweze kutunga Sera ambazo zitarudisha fedha hizi kwenye mabenki ya biashara pamoja na wananchi ili maisha yaweze kuwa mazuri, lakini wananchi pia washiriki vizuri katika shughuli za kujenga nchi yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tumeshusha kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi na kwa sasa tunafanya ufuatiliaji kuona kwamba, riba zinazotozwa na benki zetu za biashara pamoja na taasisi za kifedha zinashuka ku-respond katika jitihada hizi ambazo zimefanywa na Serikali kupitia Benki Kuu. Tutakapomaliza ufuatiliaji huu na sasa hivi tuko katika vikao mbalimbali na mabenki haya kuona ni jinsi gani sasa wanaweza kurejesha riba chini ili wananchi wetu waweze kukopa, tutaleta taarifa katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, napenda kumwambia Mheshimiwa Mathayo kuwa ni sahihi kwamba asilimia 30 tu ya pesa ndiyo iko benki, asilimia 70 iko kwa wananchi. Kinachoonekana kwa sasa ni kwamba Serikali tumeimarisha mfumo wetu wa ukusanyaji wa kodi. Yule mfanyabiashara aliyekuwa akifanya biashara bila kulipa kodi akijidanganya ile ni faida yake, sivyo ilivyo kwa sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Waheshimiwa Wabunge mtuunge mkono tuweze kukusanya kodi inavyostahiki na ili Watanzania sasa tuishi katika uchumi ambao Taifa letu na wananchi wanastahili kuishi. Kiuhalisia fedha bado iko ya kutosha katika mikono ya wananchi kama alivyokiri yeye Mheshimwa Mbunge aliyeuliza swali kwamba asilimia sabini ya pesa yetu iko kwa wananchi na uchumi wetu unaendelea vizuri.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kumekuwa na tafsiri ambayo siyo sahihi sana kwa vijana ambao wananunua Kwacha kwenye mpaka wa Tunduma na Zambia ambapo fedha hizo, Wazambia wanapokuwa wamekuja kununua bidhaa kwenye Mji wa Tunduma wanakuja na Kwacha na baadaye vijana wananunua zile Kwacha na Serikali imekuwa ikisema kwamba vijana wale hawalipi kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kununua zile Kwacha, wanakwenda Lusaka kununua dola na baada ya kununua zile dola wanakuja ku-change kwenye benki zetu za Tanzania. Hawa wafanyabiashara wa Kwacha wanakuwa tayari wamelipa kodi.
Je, Serikali haioni kwamba nao pia ni walipa kodi katika Taifa hili na badala yake wanaendelea kuwasumbua? Wataacha lini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, katika mipaka ambayo kuna black market ya kutisha ndani ya Taifa letu ni mpaka alioutaja wa Tunduma na ndiyo maana wiki iliyopita Mheshimiwa Waziri wa Fedha alikuwa mpakani kule na sasa tumeimarisha na tutahakikisha Mheshimiwa Mwakajoka tunakusanya kodi yote. Hawawezi kutoa Kwacha huku wakaenda kuibadilisha na wakarudi nchini bila kukusanya kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeapa kulinda na kuweza kukusanya kodi yetu, tutaikusanya kodi hii kwa kila mtu anayefanya biashara hii. (Makofi)
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwa kuwa uhusiano wa benki na mtu wa kawaida ambaye hafanyi biashara, ni kuweka hela yake ili apate faida na pia kwa usalama; na sasa hivi tunashuhudia kwamba hata mitandao ya simu mtu unaweza ukawekeza hela yako. Ni lini sasa benki hizi zitakaa chini na kuona kwamba kuna umuhimu wa kuongeza faida (interest rate) kwa wale wanaoweka hela zao kwenye savings account?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimekuwa nikisema tangu mwaka 1991 nchi yetu iliingia katika soko huru katika masuala ya kifedha nchini na interests zinazopangwa na mabenki yetu katika savings accont huwa zinawekwa kulingana na uhalisia wa soko. Ina maana faida inapatikana kwa mabenki na kwa wananchi. Kwa kumbukumbu ambazo tunazo Wizara ya Fedha na Mipango, interest hii imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe angalizo kwa mabenki yetu kuangalia kwamba wana balance interest wanayotoza waone interest wanayowapa wananchi kwa kuweka pesa hizi katika akaunti zao hasa savings account.
Mheshimiwa Naibu Spika, nina uhakika katika hili mabenki yetu yanafanya kazi vizuri kuhakikisha wao wanapata na wateja wao ambao ni wananchi wanapata vizuri kwa kuwa tupo katika soko huria na wanapambana kuweza kupata wateja kuweka pesa katika benki zao.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Naipongeza sana Serikali kwa hatua inayochukua ili kuweza kuboresha usimamiaji wa rasilimali zetu.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa uwepo wa Kamati za Ukaguzi ni muhimu sana katika kuimarisha mfumo wa udhibiti katika taasisi hususan katika Halmashauri zetu. Kwa kuwa Kamati imara husaidia Maafisa Masuuli kutimiza wajibu wao na hii Kamati ni muhimu kwa ajili ya kusimamia pia mpango kazi wa Wakaguzi wa Ndani na Wakaguzi wa Nje. Kwa kuwa Serikali imetoa mwongozo wa mwaka 2013 na haujatekelezwa vizuri katika Halmashauri zetu.
Je, Serikali iko tayari kuzielekeza upya Halmashauri zetu kutekeleza mwongozo huu mzuri kikamilifu ili kuleta tija zaidi katika usimamiaji wa rasilimali zetu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake katika kuhakikisha rasilimali za Taifa letu zinatumika ipasavyo na kama ailivyouliza, sisi kama Wizara tupo tayari na tumekuwa tukihakikisha Kamati hizi zinatekeleza maelekezo na miongozo yote inayotolewa na Wizara ya Fedha.
Mheshimiwa Spika, sasa kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba tunaendelea kushughulikia sheria hii pamoja na kanuni zake ili tuje na sheria itakayohakikisha rasilimali za Taifa letu zinasimamiwa ipasavyo.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa Serikali inakiri kwamba baada ya TRA kupokea jukumu hili mapato yameongezeka ukilinganisha na Halmashauri za Wilaya; na kwa kuwa Serikali mnapaswa kurudisha fedha hizo katika Halmashauri kwa wakati.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha 2017/2018 Serikali imefuta vyanzo vingi vya Halmashauri ambavyo vilikuwemo kwenye bajeti ikiwemo ushuru wa mabango, makanyagio, ushuru wa mazao chini ya tani moja, farm gate price kutoka asilimia tano mpaka asilimia tatu na kwa kiwango kikubwa uendeshaji wa Halmashauri zetu unategemea fedha za ndani (mapato ya ndani).
Je, Serikali sasa baada ya kufuta vyanzo hivi vingi ambavyo kwa kiwango kikubwa inaharibu utekelezaji wa bajeti zetu katika Halmashauri. Ni lini mtahakikisha fidia ya vyanzo hivi inatolewa na Serikali Kuu ili Halmashauri zetu ziendelee kufanya kazi kwa ufanisi? (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nafuta na nauliza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imekuwa ikichelewesha fedha mmekuwa mnasema mnakusanya TRA na baadaye fedha zitarudishwa kwenye Halmashauri. Kwa kuwa mmekuwa mkichelewesha. Sasa ni lini mtaacha kuchelewesha ili fedha hizi ziende kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwanza kwa kurekebisha Kiswahili kile lakini sio kosa lake ni kosa la watani zangu hawa wa Manyara, lakini nashukuru umerekebisha sasa imekaa vizuri.
Mheshimiwa Spika, nianze kusema kwamba kwanza Serikali haipendi kuchelewesha fedha hizi kupeleka katika Halmashauri zetu. Tunachofanya Wizara ya Fedha tunasimamia mpango wa cash budget, tunakusanya na tunapokusanya tunahakikisha Halmashauri zetu zinapatiwa fedha kulingana na bajeti zao ambazo zimetenga.
Mheshimiwa Spika, hii inakwenda katika swali lake la pili alilosema tumefuta vyanzo vingi, lengo letu kama Wizara, kama Serikali, ni kuhakikisha tunapeleka unafuu wa maisha kwa wananchi wetu. Usumbufu wa kodi mbalimbali na ushuru ambao walikuwa wakisumbuliwa ndiyo ambao Mheshimiwa Rais wetu aliahidi kufuta na sisi kama Wizara tumesimamia na tumefuta.
Mheshimiwa Spika, kama Wizara niseme hatujawahi kuacha kupeleka bajeti kwa halmashauri zetu pale ambapo fedha yetu imekuwa inatosha. Tunapeleka na tunaahidi kuendelea kuzipelekea halmashauri zetu bajeti zao kama ambavyo zimepitishwa na Bunge lako tukufu, na nimhakikishie Mheshimiwa Cecilia kwamba halmashauri zote zitapata bajeti zao kama ambao zimepitishwa. Na hii ni dhamira yetu na tumeanza utekelezaji, na yeye ni shahidi kule kwenye halmashauri yake anaona jinsi ambavyo tunapeleka fedha hizi kwa sasa.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi niulize swali la nyongeza. Wakati tunapitisha bajeti tuliongelea suala la kodi ya majengo kwamba nyumba za kawaida zitaanzia shilingi 10,000 na nyumba ambazo zinakuwa kwenye level ya maghorofa zitaanzia shilingi 50,000. Lakini cha kushangaza mpaka sasa hivi tunaona kodi hizi hazina uwiano, unakuta kati ya nyumba na nyumba mwingine anapelekewa kodi ya shilingi 10,000 mwingine shilingi 30,000, mwingine shilingi 40,000.
Je, nini kauli ya Serikali kuhusu hizi kodi na uwiano ambao si sawa kati ya Halmashauri ama Manispaa ndani ya Manispaa moja unakuta kata nyingine bei ni tofauti na kata nyingine bei ni tofauti, ama Halmashauri moja ni bei tofauti na Halmashauri nyingine ni bei tofauti.
Je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na kodi ambayo tuliipitisha sisi wenyewe Wabunge wakati wa bajeti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kodi aliyoiongelea ya majengo inayokusanywa tofauti kutoka halmashauri moja kwenda halmashauri nyingine ni kodi iliyopitishwa na Bunge lako tukufu kwa ajili ya mwaka 2016/2017, ndiyo hiyo ambayo inakuswanywa na inaonekana kuna utofauti kutoka Halmashauri moja kwenda nyingine, kodi ambayo Bunge lako tukufu imeipitisha mwaka huu wa 2017/2018 ni kama alivyosema Mheshimiwa Dkt. Kikwembe; kwa nyumba za kawaida ni shilingi 10,000 na nyumba za ghorofa kama ambavyo ilielezewa kwenye Finance Act ni shilingi 50,000. Kwa hiyo, utofauti unaoonekana ni ile tu wananchi wetu walichelewa kulipa kodi ya majengo ya mwaka 2016/2017 lakini kwa mwaka 2017/2018 kodi itakayotozwa ni kama ambavyo Bunge lako Tukufu limepitisha.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Waziri, katika Bunge la Bajeti lililopita, tulipitisha au tulirekebisha Sheria ya Serikali za Mitaa kuhusu ushuru wa mazao; chini ya tani moja wakulima hawa wasitozwe, hasa mazao ya chakula, mfano mahindi na mazao mengine. Lakini Wakurugenzi na Mawakala katika halmashauri zetu wameendelea kuwatoza wananchi ambao wana magunia matano, matatu ya mahindi, mfano Geti la Galapo katika Halmashauri ya Wilaya ya Babati – na hilo Geti la Galapo unalifahamu mtani wangu.
Nini kauli ya Serikali kuhusu ukaidi huu wa Wakurugenzi na Mawakala kuendelea kuwatoza wakulima wetu hata magunia matatu ya mahindi wanalipa ushuru huo wa mazao, nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, sheria inabaki kuwa sheria na tunawataka wasimamizi wa sheria hii kule kwenye halmashauri zetu ambao ni Wakurugenzi wetu Watendaji wa Halmashauri zote kuhakikisha sheria hii inasimamiwa, mazao yetu yote ya biashara pamoja na ya chakula chini ya tani moja hayatakiwi kutozwa ushuru wowote, na hii ni sheria naomba itekelezwe. Na kama kuna jambo specific ambalo limetokea niwaombe sana wananchi wetu tuwasiliane. Namba zetu ziko hewani, ofisi zetu ziko wazi, tuwasiliane ili kuhakikisha sheria hii inatekelezwa kama ilivyopitishwa na Bunge letu Tukufu.
MHE. RUKIA KASSIM AHMED: Mheshimiwa Mwenyekiti,asante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri lakini bado nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali inahimiza wananchi waweke fedha benki badala ya kuweka majumbani na kwa kuwa katika jibu lako la msingi umesema kwamba malipo ya wateja hawa yatatokana na mauzo ya mali, makusanyo ya madeni na fedha zilizowekezwa katika taasisi nyingine.
Je, itakapotokea fedha za wateja ni nyingi kuliko makusanyo yaliyokuswanywa, Serikali itawasaidiaje wateja hawa ambao wao hawana makosa hasa ukizingatia kwamba benki hii ina matawi katika nchi nyingi tu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Bodi ya Akiba ya Amana wamesema kwamba hata kama mteja ameweka fedha za kigeni atalipwa fedha ya kitanzania tena kwa rate ambayo ilianza ufilisi yaani tarehe 8 Mei, 2017. Je, Serikali haioni kama huu ni uonevu na ipo haja ya kuingilia kati ili dhuluma hii isitendeke? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema malipo ya wateja yanalipwa kutokana na Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 kifungu cha 39. Kwa hiyo, kinachofanyika ni utekelezaji wa sheria hii na wala Serikali haina mpango wa kumuonea mteja yeyote. Nimesema madeni yatakusanywa na pesa hizo zitakusanywa. Serikali inasimamia hili kwa kiwango kikubwa na ndio maana mpaka leo tayari wameshaanza kulipwa wateja wote hawa zaidi ya wateja 695 wameshalipwa kiasi cha shilingi milioni 727,988,000. Ni Serikali yetu italisimamia hili kwa umakini mkubwa na kila mteja atapata amana yake kama ilivyowekezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa walioweka fedha za kigeni, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi tunatekeleza kazi hii kulingana na sheria yetu ya fedha na tutalisimamia hivyo. (Makofi)
MHE. MACHANO OTHMAN SAID: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuuliza swali moja la nyongeza lenye (a) na (b).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Benki ya FBME haikufilisika na Serikali ilitambua kwa muda mrefu kwamba inatakiwa kufungwa. Na kwa kuwa wateja wake wengi walikuwa hawajapata habari ya mwanzo. Serikali haioni kwamba ilifanya uzembe ili kuwatahadharisha wateja wao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wafanyakazi wa FBME ambao mpaka leo hawajajua hatima zao. Je, Serikali inataka kutuambia nini kuhusu suala hili. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja tu la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilitoa tahadhari kipindi kirefu sana na jinsi mchakato mzima ulivyoendeshwa ulikuwa wa huru na haki na wateja wote walikuwa wakifahamu nini kinaendelea ndani ya benki hii. Kama Serikali nimesema tunaendelea kusimamia sheria zetu zinazosimamia uendeshaji wa mabenki pamoja na taasisi zote za kifedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia BOT tumeendelea kutoa tahadhari kwa wateja wetu pale ambapo inaonekana mwenendo wa benki yoyote au taasisi yoyote ya kifedha haifanyi vizuri. (Makofi)
MHE. CATHERINE N. RUGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ili na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu kubwa ya benki kutofanya vizuri au kuwekwa mufilisi husababishwana non- performing loans au mikopo chechefu. Hesabu za Benki ya Wanawake za mwaka 2015/2016 zinaonyesha asilimia 80 ya mikopo ni mikopo chechefu (non-performing loans). Ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha inainusuru benki hii ili isiende kuwekwa mufilisi ili iweze kuwasaidia wanawake wa Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, uendeshaji wa benki na taasisi zote za kifedha hufuata Sheria ya Mabenki na Taasisi za Kifedha ya mwaka 2006. Nimesema Benki Kuu imekuwa ikisimamia taasisi zote hizi za kifedha kuhakikisha zinafanya vizuri. kutokana na tatizo la mikopo chechefu, Benki Kuu ya Tanzania imewaandikia na kutoa mwongozo kwa taasisi zote za kifedha kuhakikisha kwamba wanakuwa na mkakati na mkakati huo unawasilishwa Benki Kuu ya Tanzania ya jinsi gani wanashughulikia tatizo hili la mikopo chechefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hicho ndicho kinachoendelea kwa sasa kwa sasa mabenki yote yamekuwa makini katika kuhakikisha wanatoa mikopo kwa ajili ya nini na kwa nani kuzingatia na vigezo walivyojiwekea. Kama Serikali tuna uhakika kwamba tizo hili la mikopo chechefu litaondoka baada ya mabenki yetu na taasisi zetu za kifedha kuongeza umakini katika utoaji wa mikopo. (Makofi)
MHE. WILFRED M. LWAKATARE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Serikali iliyoyatoa hapa, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na takwimu kubwa alizozitoa ambazo zinaonyesha kupanda kwa mapato ni ukweli usiopingika kwamba yapo maeneo mengi kwelikweli ambayo hayajafikiwa na TRA kwa sababu ya mtandao wake mdogo, kiasi kwamba TRA hata kufanikisha hiki kilichofanikisha imelazimika kuwatumia Maafisa Watendaji wa Kata ambao ni waajiriwa wa Halmashauri hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini Serikali isichukue wazo langu la kujaribu kuweka category mbili kwamba baadhi ya tozo hii ya property tax na hasa za majumba makubwa zitozwe na TRA lakini kwa majengo ya chini yatozwe na Halmashauri zetu na hiyo itaongeza ufanisi badala ya kuzi-tight kwenye Majiji 30? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; suala la mapato na makusanyo kupanda limekuwa ni wimbo wa kila siku, kutoka kwenye taarifa za Serikali pamoja na TRA, lakini Bunge kupitia Kamati zake na kupitia kwenye Halmashauri zetu…
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini taarifa zinaonesha Taasisi nyingi za Serikali na Serikali yenyewe na Mashirika pamoja na Halmashauri zetu hata Bunge lenyewe limeshindwa kwenda sambamba na bajeti kiasi kwamba maeneo mengine ina-read zero, zero wakati wanasema wanakusanya sana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpomngeze kwa kukiri kwamba anaelewa sasa mapato ya Serikali yamepanda katika nyanja zote kwa kodi zote zinazokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania ikiwemo kodi ya majengo, nakupongeza sana shemeji yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hili alilolisema sasa tugawanye kwamba majengo makubwa yakusanywe na Mamlaka ya Mapato na madogo yakusanywe na Serikali za Mitaa, tutajikuta tunatumia nguvu za aina mbili katika eneo moja bila sababu yoyote ya msingi. Serikali yetu na Bunge lako Tukufu tulipitisha Sheria ya Fedha, kwamba kodi ya majengo ikusanywe na Mamlaka ya Mapato kwa lengo la kuimarisha ufanisi wake katika ukusanyaji na ufanisi wake katika matumizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali tutaendelea kusimamia sheria hii kuhakikisha kwamba lengo la kuchukua kodi hii linafikiwa na wananchi wetu wanapata huduma stahiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kwamba sasa bajeti hai-reflect mapato. Ni siku mbili zilizopita Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI amesema tangu Serikali ya Awamu ya Tano imeingia madarakani kwa mwaka huu wa fedha kwa robo tu ya kwanza Mamlaka za Serikali za Mitaa zimepata zaidi ya shilingi trilioni moja katika bajeti zao. Serikali inafanya vizuri kwenye ukusanyaji lakini pia tunafanya vizuri kupeleka fedha hizi katika kila taasisi ya Serikali yetu. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kunipa nafasi nimuulize mtani wangu swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha amesema kwamba Serikali inapeleka fedha katika Halmashauri zetu na fedha wanazopeleka kwa upande wa OC ni fedha za mitihani tu. Mfano, Halmashauri yangu ya Mji wa Babati wamepeleka 265,605,000 za mitihani tu, hakuna fedha za OC. Je, nini kauli za Serikali kuendelea kudumaza Halmashauri zetu, Wakurugenzi wanashindwa kuendesha ofisi na ni lini wanapeleka pesa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze pia kwa kumpongeza kwa kukiri kuwa tunapeleka fedha kwenye Halmashauri. Kwa sababu swali hili linahitaji takwimu nitamletea takwimu sahihi katika Halmashauri yake tumepeleka kiasi gani kama OC katika utekelezaji wa bajeti. (Makofi)
MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nasikitika kwa majibu ya Serikali kwasababu vifaa vya ujenzi hata vikijenga barabara, vikijenga kila kitu mwisho wa siku ina mahusiano ya moja kwa moja na maisha ya wananchi wa kawaida. Barabara hizi zimekuwa zikijengwa kwa gharama kubwa na wananchi ndio wanalipa kodi kwa hiyo Serikali hii haioni bado kuna sababu ya kuwapunguzia wananchi wake mzigo kwenye gharama ya vifaa vya ujenzi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pilli katika zile basic human needs kuna nyumba, mavazi na kuna chakula na heshima ya binadamu yoyote ni mahali anapokaa kwa maana ya makazi. Na nchi nyingine zimeenda mbali kuwapatia wananchi wake makazi hata ya bure, Serikali yenu ya CCM inaona ni muhimu zaidi kutoza kodi kuliko maisha ya wananchi ambao wanaishi kwenye maisha duni na makazi duni?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi na naomba ifahamike kwamba uhai wa Taifa lolote ni kodi hakuna maendeleo ya Taifa lolote bila kodi na kama nilivyosema wafanyabiashara wapo wengi wanafanya kazi hizi na kusema kwamba hapa tunasamehe kwa sababu wanakwenda kujenga nyumba ni watu wa kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, niulize tu swali na mimi labda hivi kabla ya kodi hii ya VAT mwaka 1998 wananchi walikuwa wakijenga tofauti na wanavyojenga leo baada ya kuwa tunakodi ya VAT? Hiyo si sahihi hata kidogo hali ya ujenzi ipo na sasa hivi tunaona Watanzania wengi wameinuka kimaendeleo na wanajenga nyumba za kudumu kwa asilimia kubwa kuanzia mijini mpaka vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu makazi ya bure anayosema Mheshimiwa Heche, makusanyo ya kodi ndio yatakayosababisha tutoe huduma kwa wananchi wetu, na sisi tunapoelekea ndio huko huko inawezekana kabisa tukafika sehemu baada ya kuimarisha makusanyo ya kodi ikiwepo kodi ya VAT tukaweza kutoa huduma nyingi kwa wananchi wetu bure lakini kwa kuzingatia kwmba uhai wa Taifa lolote ni kodi na hakuna maendeleo bila kodi.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwanza nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri kwamba uhai wa Taifa ni kodi. Lakini kuna kodi inakuwa-charged mara mbili ya VAT kwa bidhaa hizo za vifaa vya ujenzi ambavyo vinakwenda Zanzibar kwa wale ambao non registered for VAT. Je, Serikali ina maelezo gani juu ya kutatua kero hii ya double VAT?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza si sahihi kusema kodi inalipwa mara mbili kwa kutoka Tanzania Bara kwenda Tanzania Zanzibar si sahihi. Kodi ya VAT ni kodi ya mlaji inayolipwa na malaji wa mwisho na kodi hii inakuwa-charged mara moja tu, kodi ambayo najua ina changamoto ya kusema kwamba ina sura ya kulipwa mara mbili lakini kiuhalisia hailipwi mara mbili ni kodi ya import duty ambayo kwa wenzetu Wazanzibari wanapoingiza bidhaa kule Zanzibar mfumo wanaotumia haulingani na mfumo wa Tanzania Bara.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo na ile pia hatuwezi kusema ni double taxation ile ni kuhakikisha kwamba kunakuwa na usawa katika soko wa bidhaa zinazoingizwa kutoka nje ya nchi.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Kwa kuwa Serikali inatoza VAT kwenye vifaa vya ujenzi lakini pili tena tuna suala zima la tozo kwenye majengo, je, Serikali haioni sasa kuna sababu ya kumtoza mwananchi huyu kodi moja tukaondoa ya majengo tukabaki na hiyo tozo ya vifaa vya ujenzi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kodi hizi mbili ni kodi tofauti kabisa huku tuna- charge kodi ya VAT kwa mlaji wa mwisho na hasa ambaye yuko registerd kwa VAT, ambaye anavuka mapato yake kwa shilingi milioni 100 na kodi ya majengo hii ni kodi tofauti kabisa wala hazina sababu ya kuunganishwa pamoja. Mheshimiwa this isproperty tax na hii ni kodi ya mlaji, ka hiyo, kodi hizi haziwezi kuunganishwa na ikawa kodi moja.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeamua kuuliza swali hili kwa sababu ya msingi, kwanza, naomba nieleze, mimi ni Mwalimu kitaaluma na mada hii ya shilingi na senti inafundishwa katika shule zetu za msingi.
Kwa kuwa inafundishwa katika shule zetu za msingi, zana ni sehemu muhimu sana katika ufundishaji kwa mwalimu na ujifunzaji kwa mwanafunzi. Hii hupelekea kufanya somo lieleweke kwa ufasaha na kwa urahisi zaidi badala ya kutumia maneno mengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuondoa hizi senti, ninaamini kwamba mtoto huyu wa Kitanzania ambaye hajui hizi senti ni kumwekea wakati mgumu sana na siyo kwa mwanafunzi tu bali hata kwa mwalimu.
Je, Serikali haioni kwamba mtoto huyu ananyimwa haki yake ya msingi ya kuzijua hizi senti? Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, umesema kuondoa na kuweka sarafu zenye thamani kubwa kunaimarisha mfumuko wa bei, lakini naomba mtambue kwamba hakuna bilioni moja isiyoanzia na senti tano. Shilingi bilioni moja ni lazima ianzie na senti tano. Hata bajeti zinapokuja tunaambiwa kwamba bajeti hii ni ya Shilingi bilioni moja na senti kadhaa. Sasa tunapoondoa tunaweka uhalisia gani wa senti yetu hiyo ambayo ni senti tano? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua fika kwamba mtoto huyu wa Kitanzania anatakiwa kufundishwa na ndiyo maana mada hizi zipo katika shule zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika jibu langu la msingi namba (b) nimesema kwamba, fedha hii bado ni halali kwa matumizi halali ndani ya nchi yetu na Serikali kupitia Benki Kuu haijaziondoa fedha hizi sokoni, bado fedha hizi zipo na zinapohitajika zinapatikana kwa matumizi husika.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi niulize maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru kwa majibu ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri ameyatoa kwa sababu mengi ni ya ukweli. Ni kweli nyumba nyingi hazijafanyiwa uthamini lakini zinatozwa hizo kodi na kodi zinazotozwa ni kwamba siyo zile tulizopitisha za shilingi 10,000 wala shilingi 50,000 ni zaidi ya shilingi 300,000 kwa nyumba ambazo hazijafanyiwa uthamini. Kwa hiyo, nashukuru kwa jibu lake ambalo amelisema ni la ukweli.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye swali langu, kwa kuwa nyumba nyingi za watu binafsi hazina BoQ kwa sababu wanajenga kwa kujidunduliza, leo mwananchi akipata shilingi 50,000 anasema ananunua cement, kesho kutwa akipata shilingi 100,000 atanunua bati, haweki kwenye kumbukumbu kwamba mwisho wa siku ametumia shilingi ngapi; na hiyo nyumba Serikali haifanyii uthamini, lakini kesho inampelekea bili ambayo wao uthamini wao aidha ni wa macho ama ni wa nini, bila kuangalia kumbukumbu za yule mtu binafsi.
Je, Serikali inasema nini na inatoa mwongozo gani thabiti kwa kutoa majawabu ili wananchi hawa ambao ni kama mimi binafsi, ambaye siweki kumbukumbu, nimejenga nyumba na leo nakuja kufanyiwa uthamini ambao ni zaidi ya pesa ambayo nakuwa nimeweka? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize swali la pili, tangu utaratibu huu umeanza, je, Halmashauri zimefaidika kwa kiasi gani? Kwa sababu sehemu ya Halmashauri sasa hawakusanyi mapato, mapato yanakusanywa na TRA na pia majengo mengi, maboma yako kwenye Halmashauri huko ambayo ni zahanati na mashule. Kwa mfano, kwenye Jimbo langu la Kavuu kuna maboma ya shule 69 hayana mabati mpaka kesho, Halmashauri zimefaidikaje na hizi pesa zinazokusanywa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwenza kuhusu uthamini wa nyumba, uthamini wa nyumba unafanywa na wathamini wenye weledi mkubwa na hivyo thamani inayoelezwa ya kila nyumba imefanyiwa na wathamini hawa wenye weledi kwenye kazi yao na wenye uzoevu wa kutosha. Hivyo kila jengo linapewa thamani yake kulingana na bei ya soko la jengo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu Halmashauri zimefaidikaje? Napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba madhumuni ya kodi hii ya majengo kuhamishiwa kwenda Mamlaka ya Mapato Tanzania ilikuwa ni kuleta ufanisi katika ukusanyaji, lakini pia katika matumizi ya kodi hii ya majengo. Lengo la Serikali ni jema na kwenye ufanisi tunafanya vizuri. Kuanzia Julai mpaka Desemba tumeshakusanya zaidi ya shilingi bilioni 16.7 na kulingana na sheria yetu ya fedha ilivyoletwa na kupitishwa na Bunge lako Tukufu, ni kwamba pesa hizi zitarejeshwa kulingana na bajeti za Halmashauri husika zilizopitishwa na Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu kwa nia njema inafanya hayo yote.
MHE. GIMBI D. MASABA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa Watanzania zaidi ya asilimia 65 wanategemea kilimo cha mikono; na kwa kuwa kilimo kimechangia asilimia 29.1 sawa na dola za Kimarekani bilioni 13.74 kwenye pato la Taifa yaani GDP ya mwaka 2016/2017...
e, Serikali haioni kwamba umefika wakati sasa wa kuondoa kodi na tozo zote kwa zana za kilimo hasa matrekta pasipo kuwepo na ukomo kama ilivyo kwa sasa? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa wananchi wengi Tanzania wana matamanio ya kupata matrekta kwa wingi, je, Serikali haioni kwamba inatakiwa ihamasishe kupata viwanda vya kuunganisha matrekta ili wananchi walio wengi waweze kuyanunua kwa wingi ili kuweza kuboresha kilimo cha kisasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lako Tukufu ni shahidi, katika kipindi cha mwaka huu wa 2017/2018 Serikali kwa kutambua umuhimu wa wakulima na mchango wao mkubwa kwenye pato la Taifa, iliondoa kodi na tozo mbalimbali ambazo zilikuwa zinamsumbua mkulima na hii ni dhamira njema ya Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondoa kodi hizi ni mchakato wa kisheria na Serikali ya Awamu ya Tano tumekuwa tukimsikia Mheshimiwa Rais wetu akisema, yuko tayari kabisa yeye na Serikali yake kuhakikisha kodi zote zile ambazo ni sumbufu kwa wakulima zinaondolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeanza 2017/2018 kuondoa zaidi ya kodi 15 kwa wakulima wetu na tunaendelea na mchakato sasa wa Sheria ya Fedha ya mwaka 2018/2019. Dhamira ya Serikali ni njema tu tutaendelea kutekeleza hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kutoka kwenye ukomo huo, Serikali inatambua. Tuliweka ili kuangalia mazingira ya ufanyaji kazi, tunaendelea kulishughulikia na litakaa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili kuhusiana na viwanda vya kuunganisha matrekta, naamini Mheshimiwa Waziri wa Viwanda yuko hapa na amekuwa akisema vizuri. Tayari tuna kiwanda pale Kibaha cha kuunganisha matreta, tumeanza kutekeleza dhamira ya Serikali ili kuhakikisha kilimo chetu kinaongeza uchangiaji wake katika pato letu la Taifa na kuwawezesha Watanzania walio wengi katika shughuli hii muhimu kwa Taifa letu. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni wajibu wa Serikali kuhakikisha wananchi wake wanapata pembejeo za kutosha na wanapata masoko ya uhakika, jambo ambalo Serikali hii imeshindwa kutimiza wajibu wake.
Swali langu, Serikali ina mkakati gani wa kuandaa masoko ya uhakika badala ya taabu ambazo wanazipata wananchi wetu na kupata umaskini unaosababishwa na Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nikanushe kwa herufi kubwa kwamba Serikali imeshindwa kutengeneza mazingira kwa ajili ya watu wetu. Hiyo ni uongo kabisa na ndiyo maana suala la commodity market kama Wizara tunaendelea kulisimamia na limefika hatua nzuri kuhakikisha sasa wakulima wetu, wafanyabishara wetu wanauza mazao yao katika soko ambalo limeandaliwa kwa umakini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme na ndiyo maana hata zao la korosho limenyanyuka na linakimbia, hii ni kwa sababu ya jitihada za Serikali yetu kuhakikisha wakulima wetu na wafanyabiashara wetu wanaweza kufikiwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. ENG. RAMO M. MAKANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza majibu mazuri ya Serikali kwa swali hili. Lakini pamoja na pongezi zangu hizo naomba kuwasilisha maswali yangu mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Kwanza takwimu zilizosomwa kwa ufupi zinaonesha kwamba kwa wastani uchangiaji wa mazao katika sekta ndogo hizo za kilimo, misitu na uvuvi ni 26.1%. Lakini pia wastani wa fedha za kigeni katika miaka hiyo mitano ni dola za Kimarekani milioni 864.68.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Taifa letu limepanda treni ya mwendo kasi inaitwa viwanda kwa ajili ya kukamilisha safari yake kuelekea uchumi wa kati inaonekana wazi kabisa, ushahidi upo unaoonesha kabisa juu ya umuhimu wa sekta hii ya kilimo, lakini mahususi kabisa mazao yale matano yaliyotajwa yaani tumbaku, korosho, kahawa, pamba na chai.
Mheshimiwa Mwenyeki, sasa maswali yangu ya nyongeza yatajikita zaidi kwa korosho kwa leo na nikisema kwamba swali la kwanza, kwa kuwa sasa tunataka mazao haya yachangie zaidi uchumi na kuongeza kasi hiyo yakufikia malengo ya Taifa ya kiuchumi. Je, Serikali inajipanga namna gani kuondoa vikwazo, kuondoa hali yoyote ile ambayo inawafanya wakulima washindwe kuzalisha zaidi? Kwa mfano kwa sasa hivi kule Tunduru wananchi wanapata matatizo ya upatikanaji…
Ndiyo, Serikali itaboresha namna gani utaratibu wa kibenki, unaowafanya Wananchi wa Wilaya ya Tunduru wapate shida katika kupata fedha zao baada ya kuuza mazao ya korosho miezi kadhaa iliyopita waondokane na misururu mirefu lakini pia na kusafiri kilometa nyingi zinafikia 120 na kukaa Makao Makuu ya Wilaya kwa siku mbili mpaka tatu? Hilo ni swali la kwanza.
Swali la pili linausiana na suala la pembejeo, upande wa pembejeo ningependa kuzungumzia ubora wa pembejeo zenyewe, lakini pia ningependa kuzungumzia upatikanaji kwa wakati wa pembejeo zenyewe, lakini pia bei ya pembejeo zenyewe. Kwa ujumla Serikali inajipanga namna gani katika kuhakikisha kwamba wananchi hawa wa Tunduru hasa wa zao la korosho, ni wa mazao yote lakini hususani wa zao la korosho kwa leo ili waweze kupata pembejeo hasa mbolea na madawa ya kuweza kuboresha, kilimo na hasa mazao ya ya korosho upande wa sulphur?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaifahamu changamoto hiyo ya wananchi wetu na hasa wakulima wetu wa kule Tunduru kwenda kupanga foleni katika mabenki yetu na hili hata Mheshimiwa Naibu Waziri wa Viwanda tarehe 10 Januari aliwasiliana na mimi akiwa Masasi, akiwa kwenye foleni na wananchi hao kwa ajili ya kupata huduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema kwamba kama ambavyo nimekuwa nikiliambia Bunge lako Tukufu kuanzia mwaka 1991 tuliingia katika soko uria kuhusu sekta ya kifedha na mabenki nchini. Lakini pia, mabenki yetu kwenda kufungua matawi maeneo mbalimbali huwa inahitaji kuangalia nguvu ya soko (demand and supply) katika hilo, maana na wao ni wafanyabiashara wanahitaji kupata faida wanapofungua matawi yao.
Ninafahamu kuhusu wakulima wetu wa korosho kule Tunduru na Mtwara kwa ujumla na Wilaya zake na zao hili ni la msimu kwa hiyo kunakuwa na wateja wa msimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokifanya kama Wizara ya Fedha kwa sasa ni kuongea na mabenki yetu kuona jinsi gani watafikisha huduma za mawakala (Agent Banking) au waweze kutumia Mobile Banking katika kuwahudumia Wananchi wetu wa maeneo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili Serikali inatambua umuhimu wa mazao yote kwa ujumla na particular mazao haya matano niliyoyasema na ndiyo maana Serikali mwaka 2013 ilikuja na Regulatory Authority ambayo ni TFRA inayoshughulika na pembejeo za wakulima wetu. Tunaendelea kuimarisha wakala huu ili uweze kufanya kazi nzuri kuhakikisha wananchi wetu wanapata pembejeo wanazozihitaji hasa katika ubora na bei ambayo wanaweza kuihimili kuinunua.
MHE. ESTER A. BULAYA: Ahsante Mwenyekiti na Mtemi wa Wanyantuzu kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa dhamira ya Serikali ya kuanzisha benki ya kilimo, ni kwa ajili ya kuinua sekta ya kilimo na kuwasaidia wakulima kwa ujumla ambao ndiyo sekta hiyo ndiyo inayochangia katika ajira pamoja na pato la Taifa. Tunajua, Benki ya Kilimo ….
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo naenda Benki ya Kilimo ina mtaji wa Bilioni 60, ili kufikia malengo ya kuwasaidia wakulima ilikuwa inapaswa kuwa na Bilioni 800, Serikali mkaji-commit kwa kila mwaka kwa miaka minane kupeleka bilioni 100, 100 lakini mpaka hivi tunavyoongea hamjapeleka.
Je, ni lini Serikali sasa mtapeleka fedha hizo kwenye Benki ya Kilimo, ili wakulima wanufaike na benki hiyo na kuhakikisha wanachanigia zaidi katika pato la Taifa na Sekta ya Kilimo kwa ujumla?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jana tu Mheshimiwa Waziri wa Fedha alisema vizuri sana kuhusu Benki ya Kilimo. Kwa hiyo, na Mheshimiwa Ester alikuwepo naamini anakumbuka na Bunge lako Tukufu linakumbuka kwamba dhamira ya Serikali yetu ni kuhakikisha kwanza tunaimarisha ufanisi wa utendaji kazi wa Benki ya Kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri wa Fedha naomba nikope maneno yako uliyoyasema jana; “Kwamba tayari tuko mchakato unaelekea mwisho wa kuhakikisha menejimenti inakaa vizuri ili pesa ya Serikali inayoingizwa kwenye benki hiyo iweze kufanya kazi vizuri na waweze kuwafikia wakulima wetu.” (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nikumbushe Bunge lako Tukufu, nimekuwa nikisema benki hii sasa pamoja na ukakasi uliopo kwenye menejimenti lakini tayari walishaanza mchakato wa kufungua matawi kwenye kanda sita ndani ya Tanzania, hii ikiwa ni dhamira ile ya dhati ya Serikali yetu yakuhakikisha benki hii inawafikia wakulima kule walipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, dhamira yetu ni ya dhati na ndiyo maana tumechukua pesa kutoka African Development Bank na kuzipeleka benki ya Kilimo. Kwa hiyo, hii bilioni moja, moja kwa miaka nane inayosemwa mbona hatuongelei hizi pesa za African Development Bank. Hizi ni pesa za Serikali pia na ndiyo maana tumepeleka ili kuiwezesha benki yetu iweze kuhudumia wananchi wetu. (Makofi)
MHE. JAMAL KASSIM ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kutokana na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ameonesha wazi kwamba transaction ambazo zinafanyika kupitia E-Commerce zinaongezeka na Mamlaka ya Mapato (TRA) hawana access ya moja kwa moja ya kuona hizi transaction ambazo zinafanyika kupitia E-Commerce;
Je, Serikali inasema nini sasa kuhusu kujijengea uwezo aidha wa ku-establish link baina ya mfumo huu wa EFDs na ule wa TCRA ambao baadhi ya transaction zinaweza kupatikana kwenye ule mfumo wa TCRA?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, suala la wataalam Mheshimiwa Waziri angefafanua zaidi anapokusudia Serikali imeamua kuongeza uwezo kwa wafanyakazi alimaanisha ni kwa namna gani?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza, kwanza kabisa naomba niseme kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi siyo kwamba hatuna access na hatuzifikii hizo taarifa hapana! Taarifa hizo tuzazifikia kwa sababu hata transaction zinazofanyika kati ya TANESCO unanunua kupitia simu yako unaoneshwa kabisa kodi ipi inalipwa wapi na inalipwa kwenda wapi, hizo zote zinakuwa accessed na mfumo wetu wa EFDs kule Mamlaka ya Mapato. Kwa hiyo, tuna uwezo wa ku-access ila nimesema changamoto za kiteknolojia zinakuwa siku hadi siku na ndipo niliposema kwa swali lake part (b) kwamba tunaendelea kuwawezesha watendaji wetu kuwapa uwezo zaidi kulingana na mabadiliko ya mifumo ya kiteknolojia yanavyotokea siku hadi siku. (Makofi)
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Naipongeza Serikali kwa kuweka mfumo huu wa EFDs kwa ajili ya kukusanya kodi ili kuhakikisha kwamba Serikali inapata mapato stahiki kulingana na biashara zinazofanyika ndani ya nchi yetu, huo ni upande mmoja wa shilingi katika kukusanya mapato.
Upande wa pili, je, ni lini Serikali sasa itaweka bei kwa kila bidhaa inayoingia nchini ili wafanyabiashara wetu wanaoingiza mali kutoka nje ya nchi ajue hasa kwamba nikiingiza gari aina fulani ya mwaka fulani inalipiwa kiasi fulani ili asikwepe kodi lakini na kumfanya mtu wa TRA kuwa na negotiation ya kodi ili Pato la Taifa liongezeke kwa mfanyabiashara wetu kujua hasa kwamba nikileta kitu hiki nakilipia ushuru huu? Kwa hiyo, yeye mwenyewe hakuna negotiation ili kuondoa mambo ya rushwa na mambo ya manung‟uniko kwa wafanyabiashara wetu. Ahsante. (Makofi)anajijua na
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, bei anazosema kwa ajili ya bidhaa zote zinazoingia nchini tunazo na ndiyo ambayo inakuwa ni base ya kuweza kufanya tax assessment kwa bidhaa zote zinazoingia. Kwa hiyo, tunazo bei hizo ambazo zinakuwa zimetumika kwa bidhaa hizo kwa muda wa miezi mitatu iliyopita, miezi sita, miezi sita ndani ya nchi yetu bidhaa hizo ziliingia kwa kiasi gani. Kwa hiyo hizo taarifa na database tunazo katika Mamlaka ya Mapato Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba tunazo hizo lakini pia Mamlaka ya Mapato huwasiliana na mamlaka za masoko mengine nje ya nchi yetu kuweza kujua bidhaa kama hizo zinauzwa kwa shilingi ngapi ili tunapofanya tax assessment kwa ajili ya wateja wetu, tuwe tunawatendea haki wateja wetu. Kwa hiyo, tunatumia njia zote hizo na database hiyo Mheshimiwa Mbunge ipo kabisa na tunaitumia.
MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nashukuru kwa majibu ya Serikali ambayo yametolewa, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Bukoba wanalima chai pamoja na mazao mengine. Wanajituma, wanaweka bidii kubwa sana kwa lengo la kukuza uchumi wao, uchumi wa familia zao na uchumi wa Taifa. Huyu mwekezaji kama jibu lilivyosema anawadhulumu wakulima hawa, hawalipi fedha zao, hawalipi haki zao; wakulima pamoja na wafanyakazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pamoja na majadiliano hayo ya mwezi Oktoba na mwezi Desemba mwaka jana, jibu linamalizia kwamba Serikali haioni saabu ya kuvunja mkataba. Kweli pamoja na dhuluma hii anayowafanyia mwekezaji huyu Serikali haioni sababu ya kuvunja naye mkataba? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli inahimiza uchumi wa viwanda, lengo ni hilo hilo kuboresha ustawi wa Tanzania, kuongeza ajira na uchumi wa Taifa. Huyu anafanya kinyume na azma ya Serikali ya Awamu ya Tano, bado wanasema hawaoni sababu ya kuvunja mkataba, kweli hii ni sawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nitakuwa mtu wa mwisho kuona Watanzania wanadhulumiwa na mimi na Waziri wangu tukiwa ndani ya Wizara ya Fedha na Mipango na ndiyo maana katika jibu langu la msingi nimesema ameshafanya malipo yote na kwa sasa yuko current kwenye malipo ya wafanyakazi lakini pia malipo ya wakulima, anawalipa kila wanapomaliza kuuza chai yao anaendelea kuwalipa.
Mheshimiwa Naibu Spika, na kilichotokea huko nyuma, Kampuni hii ya Spearshield Africa Company Limited ilinunua hisa za asilimia 75 kwenye kiwanda hiki. Asilimia 25 zilitakiwa zinunuliwe na wakulima wenyewe hadi leo hii wakulima wameshindwa kununua hizi hisa asilimia 25 na uzalishaji wao ukawa si wa tija ndiyo maana mwekezaji akawa anazalisha chini ya ufanisi, akawa anashindwa kufanya biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwekezaji huyu pamoja na kwamba makubaliano ya awali ilikuwa baada ya kuchukua asilimia 25 aweze kuweka uwekezaji wa milioni 99 za Kitanzania, lakini kwa sababu ana nia thabiti mwekezaji huyu mpaka Desemba, 2016, tayari alishawekeza zaidi ya bilioni 3.8 kwenye ununuzi wa mitambo, kwenye kilimo na kuwawezesha wakulima kwenye ukulima bora wa mazao yao, kwa hiyo ana nia thabiti ya kufanya jambo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Msajili wa Hazina sasa imempa maelekezo kwamba awe anatoa taarifa kila baada ya miezi miwili ya utendaji kazi wake, mahusiano yake na wakulima, lakini mahusiano yake na wafanyakazi, na ameanza kufanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, naomba tumpe nafasi mwekezaji huyu, ameonesha dhamira ya kutosha, amewekeza kutoka milioni 999 zilizopo kwenye mkataba mpaka bilioni 3.8 , tumpe nafasi, ana nia thabiti atawawezesha ndugu zangu, wakwe zangu, shemeji zangu na wifi zangu wa Bukoba, kwa kiwanda hiki naamini watarejesha uchumi wao kama ilivyokuwa miaka ya 1960 na 1970.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali na hatua ambazo zimechukua katika kudhibiti matumizi ya fedha za umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya eneo ambalo limekuwa na matatizo makubwa katika taasisi za umma ni eneo linalohusu ununuzi wa vipuri na matengenezo ya magari pamoja na mafuta.
Swali la kwanza, je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba wafanyakazi wote walioko katika Menejimenti za Mashirika hayo wanakopeshwa magari badala ya kutumia magari ya Serikali?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ndiye mwenye wajibu wa kukagua hesabu zote za Serikali Kuu, Serikali za Mitaa na Taasisi za Umma, lakini kwa muda mrefu tumeona kwamba hesabu za taasisi za umma, Mkaguzi Mkuu amekuwa akizipatia sekta binafsi zimekuwa zikikagua kwa niaba yake, lakini sekta hizo binafsi zimekuwa ziki-charge fedha kubwa sana ya ukaguzi. Je, ili kupunguza matumizi Serikali ina mpango gani wa kuimarisha ofisi ya CAG ili iweze kufanya kazi hiyo sawa sawa badala ya kutumia sekta binafsi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ununuzi wa vipuri na matengenezo na watumishi kukopeshwa magari, tunapokea wazo lake zuri na tutalifanyia kazi kuona ni jinsi gani utekelezaji wake ili kuona tunapunguza matumizi haya kama alivyosema kwenye magari. Tusisahau pia ni taratibu na kanuni za utumishi ndizo ambazo zinaelekeza haya yote ambayo yanatendwa na Serikali yetu, pale ambapo itaonekana inafaa tofauti na uamuzi uliopo sasa, basi Serikali yetu haitasita kufanya hivyo ili kupunguza matumizi yasiyo ya lazima kama ambavyo Serikali imekusudia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuimarisha ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, napenda kuliambia Bunge lako Tukufu Serikali yetu inatambua umuhimu wa ofisi hii ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na imekuwa ikiimarisha kila mwaka hatua kwa hatua kuhusu wafanyakazi kupewa ujuzi lakini pia kuhusu na bajeti yake. Sote ni mashahidi tumeona juzi tumepitisha bajeti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na imeongezeka kama Bunge lako Tukufu ambavyo ilipendekeza, ni imani yangu ofisi hii itakagua ofisi zetu na taasisi zote za umma pale ambapo inaonekana inafaa.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri kujaribu kueleza sheria mbalimbali za kudhibiti fedha za umma, lakini kuna changamoto moja kubwa. Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali ndio mtu pekee ambaye amekuwa akisimamia na kudhibiti hili suala la umma na kutuonesha wapi kwenye mapungufu na matumizi sahihi. Lakini Serikali imekuwa haipeleki fedha za kutosha kwa CAG ili aweze kudhibiti hizi fedha.
Je, Serikali haioni kwamba yenyewe ndio yenye jukumu la kuzorotesha Mkaguzi wa Hesabu za Serikali kushindwa kufanya kazi yake ili tuweze kujua hayo mapungufu, kwa kushindwa kupeleka hizo fedha?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu swali la pili la Mheshimiwa Hasunga kwamba Bunge hili hata wiki haijapita tangu tumepitisha Bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango, ndani yake ikiwepo bajeti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na sote tumeona commitment ya Serikali yetu katika kuiongezea ofisi hii bajeti ya kutosha. Katika taasisi zote za Serikali ni taasisi hii tu ambayo imepata bajeti yake kwa mwaka huu kwa zaidi ya asilimia mia moja. Hii ni commitment ya kutosha kabisa na tunahakikisha kwamba itaendelea kuimarishwa kama nilivyosema. (Makofi)
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia wafanyabiashara nchini iliweza kuahidi kugawa hizi mashine bure ili kurahisisha ufanyaji wa hii miamala. Je, zoezi hili limefanyika kwa kiwango gani na Serikali ina mpango gani wa kukamilisha?(Makofi)
Swali la pili dogo, sasa hivi tunafanya miamala kielektroniki kwa mfano kulipa gharama mbalimbali kama vile umeme, muda wa maongezi wa simu, ving’amuzi, kupitia kampuni za simu. Serikali itakubaliana na maelezo ya wafanyabiashara wanaoandaa mahesabu kwamba tulifanya malipo hayo kwa njia ya kimiamala?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa swali lake la kwanza ni kweli Serikali iliahidi kugawa mashine hizi na kwa sasa tumefikia hatua nzuri, maana yake tulisitisha zoezi ili tufanye tathmini ya zile mashine tulizozigawa ili sasa kuweza kugundua changamoto na fursa nyingine katika utekelezaji wa suala hili na uthamini huu unakaribia kukamilika na muda siyo mrefu tutaendelea kuzigawa mashine hizi kwa wafanyabiashara wote ambao wako registered kwa ajili ya VAT.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu malipo ya kielektroniki ni sahihi yanafanyika katika miamala ya simu kulipia malipo mbalimbali na sisi tunashirikiana na tayari tumeisha saini Memorandum of Understanding at TCRA ili malipo yote yanayofanyika kupitia simu au e-payment yoyote ile tuweze kui-truck na kuhakikisha document zote na kumbukumbu zote zinaweza kupatikana kwa ajili ya kufanya uthamini kwa ajili ya kodi. (Makofi)
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wadogowadogo wa miti ambayo inazalisha mbao na kuni wa Mkoa wa Njombe na maeneo mengine ya Mkoa wa Iringa wamekuwa wakipata usumbufu mkubwa sana wanapovuna mbao zao na kutaka kupeleka sokoni. Wakifika Iringa wanakutana na kodi nyingine au wanakutana na utaratibu mwingine kwamba lazima wawe na risiti za EFD wakati hao wakulima wamevuna mazao haya kwenye shamba lao, na wamepata kibali cha kuvuna na kodi nyingine wameishatoa, lakini wanaambiwa wawe na risiti ya EFD na hawana mashine. Wasipokuwa na risiti ya EFD wanaambiwa watoe faini ya shilingi milioni moja. (Makofi)
Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu mzuri wa kuweza kuondoa hii kero ambayo imekuwa tatizo kubwa sana kwa wakulima wetu hususani wa Lupembe na maeneo mengine wanaosafirisha mbao zao kwenda sokoni Dar es Salaam? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi na Mheshimiwa Mbunge kama atakumbuka nimekaa naye kujadili tatizo hili na tayari nimeshaelekeza Mamlaka ya Mapato Tanzania kufuatilia jambo hili, ni risiti za aina gani zinazodaiwa Iringa tu.
Kwa hiyo, naahidi kwamba hili linafanyiwa kazi, nami nilimuahidi Mheshimiwa Mbunge nikimaliza kipindi hiki cha bajeti nitakwenda Iringa kushughulikia tatizo hili. (Makofi)
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba EFD ni mashine ya kukusanya kodi na kutoa risiti, kwa maana nyingine ni device ya TRA ya kukusanyia kodi, sasa kwa nini Serikali isiwape wafanyabiashara EFD mashine bure?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, EFD ni sahihi ni kwa ajili ya matumizi ya kikodi pia kwa matumizi ya wafanyabiashara wetu ili waweze kujua kumbukumbu sahihi katika kufanya biashara zao. Katika hili ndiyo maana Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kwamba EFD zigawiwe bure, lakini tuangalie mfumo mzuri wa kuweza ku-share gharama hizi za kupata mashine hizi za EFD. Kwa hiyo, Serikali inawekeza lakini na wafanyabiashara wetu nao wanawekeza kwa pamoja ili tuweze kujenga Taifa letu.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, naomba kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Kwa kuwa Serikali imejidhatiti kukusanya mapato kwa kupitia mashine hizi za EFD, lakini kuna matatizo makubwa ya kutokuwepo kwa mtandao au mawasiliano tunapoenda kwenye vituo vya manunuzi, vinavyosababisha wanunuzi kukaa kwenye vituo kwa muda mrefu wakisubiri risiti au wakati mwingine tunakata tamaa tunaondoka bila kuwepo na risiti.
Je, Serikali ina mpango gani makini kuhakikisha kwamba inaboresha mfumo wa kukusanya kodi pamoja na kupata huduma kwa muda unaotakiwa ili kuhakikisha kwamba kile walichokikusudia kinaliletea Taifa mapato kwa maendeleo yetu? Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakiri kwamba lipo hili tatizo kwa baadhi ya wauzaji na wafanyabiashara ndani ya nchi yetu. Tatizo la kimtandao halipo kwa kiwango ambacho wafanyabiashara wanakisema, nitoe wito kwa Wabunge kama viongozi kwenye maeneo yetu tushikamane na Serikali yetu kwa sababu hakuna maendeleo bila kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tushirikiane katika kuhakikisha wafanyabiashara wanatumia mashine hizi kwa pamoja, lakini TRA wanafanya jitihada kubwa za kupita maeneo ya wafanyabiashara wetu kuhakikisha kwamba mashine hizi zinatumika na zinafanya kazi. Ni wito wangu kwenu Waheshimiwa Wabunge tushirikiane kuhakikisha hili linaweza kufanyika ndani ya nchi yetu.
MHE. JUMA HAMAD OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa ufafanuzi wa swali langu, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, Mheshimiwa Waziri amekiri kwamba Serikali inapoteza kiasi cha shilingi za Kitanzania trilioni 1.18 kila mwaka. Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Idara ya Afrika ya IMF kuhusu effect ya hizi exemptions kwa uchumi wa nchi ambazo ziko Kusini mwa Jangwa la Sahara, imebainika katika ripoti hii kwamba Tanzania ikiwa ni moja ya nchi hizo inapoteza kiasi cha Dola bilioni 1.2 hadi Dola bilioni 2.2 kwa wastani kwa mwaka ambapo hiyo ni sawasawa na kiasi cha shilingi za Tanzania trilioni 2.2 mpaka kwenda kwenye shilingi trilioni 4.6. Nataka kujua ni takwimu zipi sahihi za Waziri au za utafiti huu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ripoti hii ya uchunguzi imebainisha kwamba kivutio cha misamaha ya kodi sio tena kivutio kikubwa kwa maana ya kuwa-attract wawekezaji kuingia katika nchi. Yako mambo matatu ambayo sasa hivi wawekezaji wanaangalia sana yakiwa ni kipaumbele. Kwanza, ubora wa miundombinu. Pili, sera sahihi za fedha zinazotabirika (predictable financial and monetary policies). Tatu, utawala bora na utulivu wa kisiasa (good governance and political stability). (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, kwa sababu tax incentive siyo tena kipaumbele au vigezo wanavyoviangalia wawekezaji, haoni kwamba time imefika sasa ya kubadilisha ile Sheria ya Uwekezaji hasa Kifungu cha 38 na kubadilisha sheria zinazoanzisha Maeneo Tengefu (Economic Processing Zone, Sspecial Economic Zone and Export Processing Zones) ili misamaha hiyo itolewe kidogo sana kuliko ilivyo sasa ambapo inachukua karibu asilimia 8.3 ya bajeti yote ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza, naomba nisema takwimu nilizozisema mimi ni halali kabisa kwa sababu zimetoka katika takwimu za Serikali na naomba aziamini. Hatuna sababu ya kudanganya takwimu hizo kwa sababu tunajua madhara ya mishamaha hii ya kodi kwa uchumi wa Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, nakiri kwamba ni sahihi kivutio cha kodi sio kivutio tena lakini nimwambie tu Tanzania yetu ni nchi ya mfano katika Bara letu la Afrika na dunia kwa ujumla kwa sera zake za monitory pamoja na fiscal policies ndiyo maana wawekezaji wanaongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nilikumbushe Bunge lako, ni juzi tu wakati tunapitisha bajeti ya Wizara ya Viwanda pamoja na bajeti ya Wizara ya Fedha, Waheshimiwa Wabunge hawa hawa walikuwa wakilalamika kwamba zipo tax incentive ambazo tunashindwa kuzitoa na wawekezaji wanashindwa kuja nchini kwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii napata shaka kidogo na swali hili la Mheshimiwa Omar, lakini kama Serikali tunajua na tunafahamu misamaha hii ya kodi tunaitoa kisheria na tunaangalia mazingira ya kiuchumi ya Taifa letu, nani anakuja na kufanya nini katika uchumi wetu, lakini pia kijamii ana impact gani mtu huyu tunayempa msamaha huu na sheria zetu pia tunaziangalia kwa uhakika kabisa.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Nina swali dogo tu la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri. Ulipaji wa kodi unategemea uwepo wa ofisi za TRA katika maeneo mbalimbali. Nimekuwa nikiuliza zaidi ya mara mbili, sisi Halmashauri ya Mji wa Kasulu tumeshatoa kiwanja kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za TRA na tumewapa bure. Swali langu, kwa sababu bajeti imepita kwa kishindo, ni lini ofisi ya TRA itajengwa katika Mji wa Kasulu ili kuhudumia Wilaya nne zilizopo katika Mkoa wa Kigoma za Kakonko, Kibondo, Buhigwe na Uvinza? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza yeye pamoja na Halmashauri yake kwa kutoa kiwanja kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za TRA katika Wilaya ya Kasulu, hongereni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, niseme Mheshimiwa Waziri wa Fedha alitoa commitment kwamba ofisi hizi zitajengwa na nirudie kusema na niagize ofisi yetu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania wahakikishe ndani ya mwaka huu wa fedha 2017/2018, ofisi hizi zinajengwa katika Wilaya ya Kasulu ili kusogeza karibu huduma hizi kwa wananchi wetu.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo tu la nyongeza japokuwa kidogo linafanana na muuliza swali aliyepita. Ili kurahisisha ukusanyaji na ulipaji kodi ni kwa nini TRA isiweke vituo katika kila Halmashauri ya Wilaya ili kupunguza usumbufu mkubwa wanaopata walipa kodi? Kwa mfano, ukichukulia Mkoa wetu wa Iringa, jiografia yake ni mbaya sana inawasabisha hata watu wengine kukwepa kodi kwa sababu tu vituo vya TRA viko mbali sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi na hakuna Taifa lolote linaweza kuendelea bila kukusanya mapato, tunafahamu kabisa hilo kama Wizara yenye mamlaka ya ukusanyaji wa mapato Tanzania. Hili la kuanzisha ofisi kila Halmashauri, nilishawahi kujibu ndani ya Bunge lako Tukufu kwamba kuanzishwa kwa ofisi huwa kuna tathmini ambayo huwa inafanyika kuangalia cost and benefit analysis ya kuanzisha ofisi hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikia Mheshimiwa Mbunge, tutafanya uhakiki na tathmini hiyo kujua kama kuna uhitaji mkubwa wa kuweka ofisi hizi katika kila Halmashauri ndani ya Mkoa wa Iringa.
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Tanzania ndiyo nchi ambayo inaongoza kwa viwango vya juu vya kodi ukilinganisha na nchi ya Kenya, Rwanda na Uganda. Serikali ina mkakati gani wa kupunguza viwango hivi kwa sababu vinaathiri sana wafanyabiashara hasa wadogo wadogo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kodi za forodha ambazo zinatozwa huwa tunafuata mfumo wa kodi wa Afrika Mashariki. Kwa hiyo, si sahihi kusema Tanzania tunaongoza kwa viwango vikubwa vya kodi. Jana tu tumepitisha bajeti kuu ya Serikali, tumeona ni kwa kiwango gani tumeweza kupunguza na kuondoa kodi ambazo zimekuwa ni kero kwa wafanyabiashara wetu hasa wafanyabiashara ndogondogo.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. TRA ni chombo cha Muungano na katika suala linalowakera Wazanzibari kwa ujumla wake ni pale wanapotozwa kodi Zanzibar na wakiingia na mizigo yao Tanzania Bara wakatozwa tena kodi mara ya pili. Suala hili limekuwa ni kero moja kubwa sana na Serikali imekuwa ikilipiga danadana kwa kuliingiza kwenye misamiati kero za Muungano, mchakato lakini halifikii mwisho. Naomba Waziri anijibu suala hili la Wazanzibari kutozwa kodi Zanzibar na wanapoingia Bara na mizigo yao wakatozwa tena kodi ni lini litamalizika na kupatiwa ufumbuzi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimwambie Serikali haina dhamira ya kuwapiga danadana wafanyabishara wa Zanzibar. Nimekuwa nikisema hapa Serikali yetu iko committed katika kuwalea wafanyabiashara wetu hasa sekta binafsi kwa sababu tunajua sekta binafsi ni injini ya uchumi wa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utozaji wa kodi mara mbili na naomba niliweke vizuri sio kodi mara mbili ni kutozwa kodi ambayo iko tofauti kati ya mifumo miwili ambayo inatumika Tanzania Zanzibar na Tanzania Bara. Katika hili, Mamlaka ya Mapato Tanzania pamoja na ZRB wanashughulikia tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisimwambie ni lini kwa sababu ni suala la kimfumo, kipindi watakapokubaliana kutumia mfumo mmoja, tatizo hili litaondoka. Hili linafanyika ili kulinda tu ile fair competition katika soko letu na hili linafanyika kwa nia njema kabisa.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mfumo wa ulipaji wa fedha sasa hivi kwa wakulima wa korosho, kuanzia mwaka jana unatumika katika kulipa kwenye akaunti zao. Wakulima wameamrishwa wafungue akaunti benki ili waweze kulipwa kupitia benki. Sambamba na hilo alilouliza Mheshimiwa Mponda, Serikali haioni kwamba sasa kuna umuhimu wa hizi benki wakati wa kulipa wakulima wa korosho, wakawa wanakwenda kufanya huduma kule vijijini kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi, badala ya wananchi kuwa wanasafiri kwenda umbali mrefu. Kwa mfano pale Mchinga kwenda Lindi kwenda kuchukua fedha, wakati unajulikana kabisa leo fulani anaenda kuchukua pesa kutoka benki. Hilo ndiyo swali langu.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bobali ametoa ushauri na sisi kama Serikali tunauchukua kuona unatekelezwa vipi ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wako salama, wanapokwenda kuchukua na kupokea fedha zao kutoka kwenye malipo hayo. (Makofi)
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Mazingira ya swali hili yanafanana kabisa na hali halisi iliyopo katika Jimbo la Vwawa hasa katika Wilaya ya Mbozi. Kwa kuwa, Wilaya ya Mbozi inajishughulisha sana na kilimo na niwazalishaji wakubwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Tawi la Benki ya Kilimo ili liweze kutoa mikopo kwa wakulima hawa wa Wilaya ya Mbozi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo tumekuwa tukisema hapa, Benki ya Kilimo sasa inaelekea kufungua Ofisi za Kanda na ofisi mojawapo ya Kanda itakayofunguliwa katika Mkoa wa Mbeya, ambapo najua ni karibu kabisa na Wilaya ya Mbozi. Ni imani yangu wananchi wetu na wakulima wetu wa Wilaya ya Mbozi watapata faida za kupata mikopo nafuu kutoka katika benki hii.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwepo sera ya kudhibiti ongezeko la watu ya mwaka 1992 na kufanyiwa maboresho mwaka 2006, bado kwa maeneo ya vijijini wazazi na familia nyingi wamekuwa wanazaa watoto wengi kwa madai kwamba kila mtoto anakuja na riziki yake. Matokeo yake watoto wanaishi katika hali ya mazingira magumu na wengi wao wanaishia kuwa watoto wa mitaani kwa sababu wanakosa huduma zote muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hali hii ambayo ni hali halisi, Serikali sasa iko tayari kutangaza ukomo wa watoto katika familia angalau tano au saba ili watoto wanaozaliwa kila mtoto apate elimu inayotakiwa, apate huduma za afya, apate mambo yote ambayo anastahili katika maisha yake?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; njia mojawapo inayotumiwa na Serikali kudhibiti ongezeko la watu ni kuwepo kwa uzazi salama. Maeneo ya vijijini bado wanaopata uzazi salama ni wachache kwa sababu vituo vya afya ni vichache, zahanati ni chache hakuna mobile clinic, kwa sababu wengi wao hawapati hii huduma jinsi inavyostahili hali ambayo wanaendelea kuzaa bila kuwepo na mpango. Serikali sasa iko tayari pamoja na juhudi zote ambazo zimeelezwa kwenye jibu la msingi kuhakikisha kwamba kule ambako hakuna zahanati, hakuna vituo vya afya, kuwepo mobile clinic za kutosha na wapelekwe watalaam, pikipiki za kutosha…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio swali, kuhakikisha kwamba elimu ya uzazi salama inawafikia kina mama wote vijijini na mijini? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza kwamba Serikali kutangaza ukomo wa idadi ya watoto, napenda kumwambia Mheshimiwa Sakaya na Bunge lako Tukufu kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba suala hili la ongezeko la idadi ya watu nchini ni suala mtambuka na ni suala la kijamii. Kusema Serikali iweze kutoa tamko la watu kupata idadi ya watoto naamini haitokuwa sahihi kijamii na kulingana na tamaduni za Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili kuhusu kutokuwa na vituo katika baadhi ya vijiji vyetu tunaona jitihada za Serikali kuhakikisha kwamba vituo hivi vinajengwa katika kila Kata yetu pamoja na zahanati katika kila Kijiji. Pia kuna ongezeko kubwa la mobile clinic katika vijiji vyetu ambayo Serikali imeanza kutekeleza na ni imani yangu akinamama watapata huduma ya uzazi salama kwa wakati muafaka.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Swali langu la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri, nataka kufahamu; je, Serikali iliafiki mwekezaji huyu kukopa na kwenda kuwekeza kiwanda kikubwa nchini Congo wakati hapa nchini bado kuna uhaba mkubwa wa sukari? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili la nyongeza ni kwamba majuzi Kiwanda cha Sukari cha Mahonda kimefungwa kutokana na uhaba wa miwa. Hali hii itapelekea Zanzibar kukosa sukari. Naomba kufahamu; je, Serikali ni lini sasa itatekeleza ujenzi wa Kiwanda cha Sukari kule Rufiji kwa kutumia bonde la Mto Rufiji katika ardhi iliyotengwa katika Kata ya Muhoro, Chumbi, Mkongo pamoja na Kata ya Mbwara ili kuweza kuwatosheleza Watanzania kwa upatikanaji wa sukari ya kutosha?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Kagera Sugar mpaka leo kimeshawekeza zaidi ya dola za Kimarekani milioni 250 na kiasi kilichokopwa kwa guarantee ya Serikali ni dola za Kimarekani milioni 65; kwa hiyo kusema wamewekeza dola milioni 250, halafu wamekopa milioni 65 na kupeleka Congo, naona siyo jambo la kawaida. Na mimi nimefika mwenyewe Kiwanda cha Kagera Sugar nimejionea uwekezaji mkubwa uliowekezwa.
Mheshimiwa Spika, ni imani ya Serikali na tunatambua hivyo kwamba pesa yote iliyokopwa kupitia guarantee ya Serikali hii dola za Kimarekani milioni 65 imewekezwa yote ndani ya Taifa letu na ni moja ya viwanda vinavyofanya vizuri sana ndani ya Taifa letu, kimeajiri Watanzania wengi, kinatoa huduma za afya bure katika ukanda wote unaozunguka Kiwanda cha Kagera Sugar, kinatoa huduma za elimu bure kwa watoto wote wa wafanyakazi ndani ya Kagera Sugar na ndani ya wananchi wanaozunguka kiwanda hicho.
Mheshimiwa Spika, tuendelee kuwapa moyo Kiwanda cha Kagera Sugar kwamba wanafanya vizuri waendelee kuwekeza kwa ajili ya manufaa ya Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, napenda tu kuliarifu Bunge lako Tukufu, Serikali ipo kwenye mchakato wa kuendelea kukiwezesha Kiwanda cha Kagera Sugar ili kiendelee kuwa cha mfano ndani ya Taifa letu, kiwanda kinachomilikiwa na Watanzania halisi wenye uchungu na Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, napenda kusema kuwa Serikali ilifanya jambo jema kurejesha bonde lile lilokuwa linamilikiwa na RUBADA. Sasa hivi Serikali ya Magufuli, Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ya viwanda, tunafahamu na ndiyo maana juzi tuliwaambia ndugu zetu wa Zanzibar, Zanzibar kuna upungufu wa sukari, miwa haitoshi. Leo kiwanda kimefungwa kwa sababu miwa haitoshi kwa ajili ya Kiwanda cha Mahonda; na Serikali yetu iko tayari kabisa Mheshimiwa Mchengerwa kwenda kuwawezesha wananchi wa Rufiji kuwekeza kwenye mashamba yale tuweze kupata outgrowers wengi na kiwanda kitawekezwa. (Makofi) Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kuna kituo kidogo cha forodha katika eneo la Murusagamba Kusini mwa Wilaya ya Ngara kwenye mpaka wa Tanzania na Burundi, kituo hiki kimekuwa maarufu tangu miaka ya 1970 lakini kwa muda mrefu mpaka sasa kinahudumiwa na watumishi kutoka kituo kikubwa cha Kabanga.
Je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka sasa wa kupandisha hadhi kituo hiki ili kiweze kujitegemea kwa sababu kuna ofisi nzuri ya TRA, kuna kituo cha Polisi ni Makao Makuu ya Tarafa ya Murusagamba eneo ambalo ni strategic kwa ajili ya maendeleo. Je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka sasa wa kupandisha kituo hiki kuwa kituo cha forodha kinachojitegemea?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania inafanya tathimini ya vituo vyake vyote vya forodha na vituo vya mamlaka vilivyopo katika ofisi zetu zote ili kutambua uhitaji wa ofisi zote hizo na kwamba tutaweza kubadilisha ofisi zetu hizi. Ni dhamira ya Serikali yetu na ndio maana tumeanza kufanya tathimini na uhakiki wa nini kinachohitajika. Lakini kwa kituo alichokitaja Mheshimiwa Gashaza kuhudumiwa na watumishi kutoka kituo kingine, Serikali ndani ya mwaka huu imetoa tayari nafasi za kuajiri watumishi 52,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya watumishi 52,000 wataajiriwa watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania ili tuweze kuwapeleka katika ofisi zetu zote hasa ofisi zetu za forodha zilizo katika mipaka ya Taifa letu.(Makofi)
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Imekuwa ni kawaida kwa Seriikali kutoa matamko ambayo hayatekelezeki. Hivi tunavyozungumza, matumizi ya dola yako pale pale. Bado zipo Taasisi za Serikali ambazo zinapata huduma au kutoa huduma kwa dola.
Je, ni lini Serikali itapitia upya sheria zake na kuona uwezekano wa kulinda shilingi kama ilivyo nchi ya Kenya au nchi ya Afrika Kusini ambapo huwezi kupata huduma bila kutumia rand? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, utitiri Bureau De Change hapa nchini umeongeza mdororo wa shilingi na imekuwa kama ni vichaka vya kutakatisha fedha.
Je, Serikali haoni kama kuna haja ya kuwa na sheria mahususi za kubana Bureau De Change?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa lazima tufahamu ni Bunge hili ndilo linalopitisha sheria na hivyo kama upungufu wowote, Bunge hili litaleta mapendekezo na Bunge liweze kupitisha sheria au kufanya mabadiliko kwenye sheria zinazotumika hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tufahamu kwamba katika misingi ya kiuchumi, matumizi ya fedha za kigeni hayasababishi kushuka au kudorora kwa thamani ya fedha yoyote ile duniani.
Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tufahamu, Mheshimiwa Mbunge ametaja nchi ya Afrika ya Kusini; napenda kuliambia Bunge lako Tukufu katika fedha ambayo imepita katika misukosuko mikubwa ni fedha ya nchi ya Afrika ya Kusini pamoja na kwamba wana sheria ya kutotumia fedha za kigeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba wananchi na Watanzania waelewe kwamba yapo mambo muhimu ambayo yanasababisha misukosuko ya thamani ya fedha ya Taifa lolote, nayo ni haya yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni nakisi ya urari wa biashara; pili, mfumuko wa bei na tatu, ni tofauti ya misimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa letu limefanya vizuri sana katika hatua hizi ambazo nimezitaja; nakisi ya urari wa biashara; na ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tano inasisitiza kwenye kuongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa hapa nchini ili tuweze kusafirisha bidhaa zile ambazo zina thamani kubwa na kuhakikisha kuwa nakisi ya urari wa biashara ndani ya Taifa letu unakuwa ni mdogo na tumefika hatua nzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, naliomba Bunge lako tukufu waendelee kuipa support Serikali yetu, Serikali ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Serikali ya viwanda inayosisitiza kuongeza thamani ili tuweze kuhakikisha kwamba thamani ya shilingi yetu inakaa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa swali lake la pili, amesema utitiri wa Bureau De Change. Kama Mheshimiwa Mbunge amekuwa ni mfuatiliaji mzuri, Serikali ya Awamu ya Tano imeongeza usimamizi katika Bureau De Change. Tumefunga zaidi ya maduka 92 ya kubadilishia fedha hapa nchini ikiwa ni katika jitihada za kuhakikisha kwamba maduka haya hayawi ni vichaka vya kusafirisha fedha zetu na hayawi ni vichaka vya kutakatisha fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaendelea kusimamia, tumepewa dhamana ya kusimamia sheria mimi na Mheshimiwa Waziri wangu, sheria zote za kifedha, sheria za Taasisi za kifedha, tutaendelea kusimamia na kuhakikisha thamani ya shilingi yetu inaendelea kuimarika. (Makofi)
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza na nitakuwa na maswali mawili.
Mheshimiwa naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imefanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba inapeleka miundombinu kwenye vijiji na miji midogo. Hata hivyo, bado hakujakuwa na mbinu mbadala ambayo inaweza ikasababisha mabenki haya yakaenda kuanzisha benki katika vijiji. Napenda kufahamu, ingawa hakuna sera, sasa Serikali kwa sababu imeshafanya haya yote, ina utaratibu gani sasa kuhakikisha kwamba Benki zinapeleka huduma zao kule vijijini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kwamba mabenki mengi hasa Benki za Kilimo na Benki ya Wanawake bado hazijapata fursa ya kupeleka huduma vijijini. Mwezi huu na miezi inayofuata benki hizi zitakwenda kufungua matawi Dodoma na Mwanza, lakini bado hazijagusa katika vijiji husika ambako kuna asilimia kubwa ya wakulima na wananchi wetu wapo kule ambao wanategemea sana shughuli za kibenki.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kufahamu; je, kwa nini sasa Serikali inaendelea kuruhusu mabenki haya kuanzishwa au kufunguliwa katika miji mikubwa na siyo vijijini ambako ndiko kwenye tija?
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kukushukuru, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ameuliza kuhusu mpango mbadala.
Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba mpango mbadala upo na Serikali inausimamia vizuri na ndiyo maana katika huduma za fedha jumuishi, Taifa letu kwa Afrika nzima linaongoza kuwa na huduma za fedha jumuishi kama mpango mbadala wa kuwafikia wananchi kule walipo. Katika ulimwengu mzima, Taifa letu linachukua nafasi ya tatu kwamba linafanya vizuri katika kuhakikisha huduma za fedha jumuishi zinawafikia wananchi wetu kule walipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi ni mashahidi, kumekuwa na wakala wa mabenki yetu, kumekuwa na huduma hizi kupitia makampuni yetu ya simu, wananchi wetu tunawafikia. Kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba tuko katika soko huria katika sekta ya fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani kulazimisha mtu ambaye anakwenda kufanya biashara kwamba lazima afungue sehemu fulani. Serikali inachokifanya ni kutengeneza mazingira mazuri na ndiyo maana tunaongoza katika Afrika katika mfumo wa huduma wa fedha jumuishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu Benki yetu ya Kilimo na Benki ya Wanawake; napenda kuliambia Bunge lako tukufu kwamba kama yeye alivyokiri, mwezi huu wa tano na mwezi wa sita Benki yetu ya Kilimo inafungua tawi lake hapa Dodoma na kule Mwanza na hii ni katika jitihada za Serikali yetu kuhakikisha huduma za benki hizi ambazo zinafanya kazi moja kwa moja na wananchi wetu zinawafikia wakulima. Tuzipe nafasi benki zetu hizi tutawafikia wananchi kule walipo.
MHE. DEO F. NGALAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Shirika hili la Posta na Simu limekuwa likijiendesha kwa kusuasua sana na moja kati ya mambo ambayo yanaifanya shirika hili lisuesue ni hela za pensheni inayolipa wale waliokuwa wafanyakazi wa Jumuiya ya Afrika Mashiriki. Je, Serikali haioni sasa umeshafika wakati kulitua mzigo shirika hili ili iweze kulichukua hilo jukumu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, malipo ya pensheni kwa hawa wafanyakazi wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki inalipwa kama kawaida, lakini kuna mabadiliko ambayo yalifanyika Julai, 2015 kupanda kwa pensheni kutoka Sh.50,000 kwenda Sh.100,000, lakini kuna baadhi ya hao wastaafu hawajabadilishiwa hizo pensheni zao, mfano, Mr Mbalamwezi. Je, ni lini Serikali itawabadilishia pensheni hizo ili ziwe sawa na wenzao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu inafanya jitihada zote na kwa sasa tunapoongea na namshukuru Mheshimiwa Mbunge amekiri kwamba kwa sasa wastaafu hao wanalipwa inavyotakiwa na pale tu wanapokuwa wameshalipwa na Shirika la Posta, Shirika la Posta linapowasilisha madai hayo Hazina walikuwa wakilipwa na hakuna madai mengine yoyote ambayo yamebaki. Kwa hiyo, tupo current kila mwezi wanapokuwa wamelipa wanaleta madai na Hazina imekuwa ikifanya malipo hayo kwa Shirika letu la Posta.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba kwa sasa tusubiri mfumo huu wa kiutaratibu wa kuunganisha Mifuko utakapokamilika then Serikali itafanya maamuzi ya aidha, wastaafu hawa wahamishiwe kwenye moja ya Mifuko hii au wahamishiwe hazina moja kwa moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, kwamba ni lini watalipwa, nimekuwa nikiliarifu Bunge lako Tukufu hapa kwamba Mifuko yetu yote ilishaanza kulipa ongezeko lile la pensheni na wastaafu waliobaki kama alivyotaja ni mmoja mmoja na tumekuwa tukishughulika na kila kesi ya mstaafu anapokuja, kila mstaafu ana mambo yake tofauti ambayo yamesababisha kwa nini wasiongezewe pensheni hii na sisi tumekuwa tukishughulika nao. Kwa huyu aliyemtaja kama kweli hajaanza kulipwa tunamwomba afike Hazina na hili tutaweza kulishughulikia. (Makofi)
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Mheshimiwa Waziri kwa muda mrefu wafanyakazi wamekuwa hawapandishwi madaraja yao kwa kigezo cha uhakiki wa vyeti feki, jambo ambalo linakwenda kuathiri pensheni zao. Naomba nipate kauli ya Serikali kwa nini hawamalizi zoezi hili ili wafanyakazi hususan Walimu waweze kupandishwa madaraja na pensheni zao zisiende kuathirika baadaye?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri swali hili ni jipya wala halihusiani na swali la msingi ambalo nimelijibu. Hili ni suala la kiutumishi na naamini Waziri wa Utumishi wakati alipowasilisha bajeti yake hapa alilisema hili suala vizuri kabisa nini kimefanyika, uhakiki ulishakamilika, zipo kasoro zilizoonekana ndio maana wanamalizia uhakiki huu na ni imani yangu watakamilisha muda sio mrefu, lakini siamini kwamba imekuwa ikizuia watumishi kupanda madaraja yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema Mheshimiwa Waziri wa Utumishi atalitolea ufafanuzi mzuri na alishalisemea, kwa hiyo nimwombe kwa kauli ya Serikali sitoweza kuitoa hapa kwa sababu swali hili ni jipya.
MHE. SUZAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Naibu Waziri wa Fedha amesema kwamba wana mpango wa kufungua Benki ya Kilimo kwenye ngazi ya kanda na kwa kuwa Mkoa wa Morogoro hususan Wilaya ya Kilombero hasa Jimbo la Mlimba sasa hivi tupo kwenye ujenzi kwa kutumia mkopo katika Halmashauri yetu tunajenga Benki ya NMB Mlimba. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kupeleka dirisha katika mabenki haya ya NMB na CRDB kwa ajili ya kusogeza huduma kwa wananchi wakulima ambao wanateseka sana katika kupata pesa za kuendeleza kilimo chao badala ya kusubiri mpaka Benki ya Kilimo ikawa Kanda ya Kati?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kufungua matawi haya kikanda ni kuwasogezea wakulima huduma kule walipo na hiyo kama nilivyosema iko kwenye mpango mkakati wa Benki ya Kilimo. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba tuu-support mpango huu ili benki yetu iweze kuwasogelea wakulima wetu kule walipo katika kanda zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili la kufungua dirisha katika mabenki mengine ya kibiashara ni wazo jipya, kama Serikali tunalichukua tuone kama linaweza kufanyiwa kazi na tuweze kuli-implement.
Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba katika benki ambazo huwafuata wakulima kule walipo ni Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania. Kwa hiyo, popote pale wakulima walipo wanapokuwa wametuma maombi kwa ajili ya mkopo, Benki ya Kilimo huwatembelea wakulima hawa kule walipo. Kwa hiyo, tuendelee kuipa support Benki ya Maendeleo ya Kilimo iweze kuendelea kuwafikia wakulima wetu kwa ajili ya kuwahudumia. (Makofi)
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa maelezo ya Mheshimiwa Waziri ingawa maelezo yenyewe yanajikanganya sana. Msingi wa swali ni hatua za makusudi za kibajeti, kwa sababu Mkoa wa Kigoma kama ilivyo mikoa mingine unapata bajeti kwa mujibu wa ceiling. Sasa nina maswali mawili madogo tu ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo barabara anazozizungumza, zimesimama kujengwa. Zimeanza kujengwa tangu mwaka 2006. Barabara hizo hazijengwi tena na Wizara ya Fedha nyie ndiyo mnatoa fedha. Ni lini sasa kwa makusudi mtatoa fedha ili barabara hizi ziweze kukamilika baada ya kukaa kwa miaka 12 hazijakamilika? Hilo swali la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni dhahiri kabisa kukamilika kwa majengo ya NSSF na National Housing hakuwezi kuondoa umaskini wa watu wa Kigoma. Hoja ya msingi ni kwamba tunataka kuwe na special strategy ya mikoa hii minne ambayo iko nyuma, ndiyo hoja ya msingi iko hapo. Majengo haya yapo tu! Kwa hiyo, msingi wa hoja yangu ni kwamba Mheshimiwa Waziri atueleze ni mkakati upi wa kuiondoa mikoa hii minne katika lindi la umasikini kuweka katika mikoa ambayo ni bora zaidi kama ilivyo mikoa mingine? Hiyo ndiyo hoja ya msingi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu la msingi nimeonesha dhahiri miradi inayotekelezwa ili kuweza kuwaondoa wananchi wa Kigoma kutoka kwenye lindi la umaskini. Huwezi kuwaondoa wananchi katika lindi la umaskini bila kuwa na miundombinu ambayo nimeionesha. Ndiyo msingi wa jibu langu la msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara zilizosimama, Wizara tupo katika majadiliano, tulimaliza uhakiki na sasa tunaelekea kulipa na barabara hizi zitaendelea kujengwa kama ilivyopangwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anauliza kuhusu special strategy, napenda kuliambia Bunge lako tukufu kwamba special strategy ipo na tumeanza kuitekeleza kwa mikoa yote. Kwa Mkoa wa Kigoma aliouliza, mfano wa special strategy ni upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma ambapo ndege kubwa zilikuwa hazitui na sasa ndege kubwa zinatua, watalii wanafika kwa wakati, wawekezaji wanafika kwa wakati, wafanyabiashara wanafika kwa wakati na tunafungua uchumi wa Kigoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekamilisha kwa asilimia 100 ujenzi wa magati mawili; Gati la Kagunga limekamilika kwa asilimia 100, Gati la Kibwesa limekamilika kwa asilimia 80. Hii ni kuufanya Mkoa wa Kigoma uwe ni hub ya biashara kwa landlocked countries zinazotutegemea sisi Tanzania ili tuweze kufungua uchumi wa watu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie Mheshimiwa Mbunge pamoja na ndugu zangu wote wa Kigoma, Serikali yao ipo makini. Tunaelewa kulikuwa na shida ya bottleneck inflation na sasa tunafungua kwa kukamilisha miradi hii, ndio maana reli yetu ya kuwa kiwango cha kisasa tunakwenda kuikamilisha kufungua mikoa yetu hii. (Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Katavi na mikoa mingine ambayo imekuwa inapokea wakimbizi ni mikoa ambayo iliathirika sana kiuchumi kwa sababu nguvu yao kubwa sana ilipelekea kubeba mzigo wa wakimbizi kutoka nchi jirani na kupelekea kuwa na umasikini kwenye maeneo hayo.
Je, Serikali imejipanga vipi kusaidia maeneo ambayo yalitoa nguvu zao kubwa sana kusaidia ndugu zetu wa nchi za jirani na hali ya maisha sasa ya wananchi ambao walifanya kazi ya kuwapokea ndugu zetu wamekuwa na mazingira ya maisha duni?
Tunaomba Serikali itupe majibu, inatusaidia vipi katika mikoa hiyo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwa Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Katavi nao ni hivyo hivyo. Tumeweka vipaumbele hasa kuhakikisha tunafungua mikoa hii kwa miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini Mheshimiwa Mbunge ni shahidi kwamba miundombinu inafunguka ili wakulima wetu waweze kusafirisha mazao yao kwa haraka na nguvu zote kama Serikali tunaelekeza kwenye mikoa hii iliyoonyeshwa kwenye utafiti ule kwamba ni ya mwisho katika hali ya umasikini ndani ya Taifa letu.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Ripoti mbalimbali ikiwemo Ripoti ya MVS na REPOA inaoneesha kwamba hali ya njaa na umasikini nchini imeongezeka kwa mwaka 2018 ukilinganisha na miaka iliyopita. Je, Serikali ina kauli gani juu ya hili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napata taabu sana kusema kwamba hali ya njaa imeongezeka ndani ya mwaka 2018. Katika bidhaa zinazochangia mfumuko wa bei au inflation rate kuongezeka ni upatikanaji wa chakula. Inflation kwa mwezi wa Tatu ilikuwa asilimia 3.9. Hii ni indicator kwamba hali ya njaa kwa Tanzania haipo na mvua zimenyesha za kutosha, wananchi wetu wako katika amani kabisa ya upatikanaji wa chakula ndani ya Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa Mbunge, yawezekana taarifa anazozisoma ni za mwaka 2016/2017 kulikokuwa na shida hiyo, siyo kwa mwaka 2018.
MHE. OTHMAN OMAR. HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu aliyoyatoa. Nina maswali mawili ya nyongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Zanzibar ni mshirika wa AICC na ina haki ya kupata gawio, lakini kauli za Mawaziri zinazohusu gawio la AICC zinakinzana. Mfano, wakati Mheshimiwa Naibu Waziri anasema kwamba AICC inapeleka gawio Serikali Kuu, lakini Mheshimiwa Waziri wa Fedha wakati akijibu swali la Na. 110 katika Kikao cha Sita, Mkutano wa Kumi alisema kwamba AICC bado haijawahi kupata gawio na kwamba Joint Finance Commission wakishirikiana na Msajili wa Hazina wameunda kikosi kazi ili kuiwezesha AICC kutengeneza faida na kuleta gawio Serikali Kuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, Mheshimiwa Waziri kauli ya Waziri wa Fedha inakinzana na kauli ya Waziri mwenye dhamana. Kwa maana hiyo, gawio linalotoka AICC haliendi Serikali Kuu. Je, Mheshimiwa Waziri haoni kwamba Zanzibar sasa hivi inakosa gawio kutoka AICC toka ilipoanzishwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, AICC imekuwa ikifanya uwekezaji mkubwa sana kule Arusha kama alivyozungumza Mheshimiwa Waziri, lakini imeshindwa kuwekeza katika mazingira ya Zanzibar pamoja na kuwa mazingira yake yanaruhusu.
Mheshimiwa Naibu Waziri, anaweza kutueleza kwa sababu gani AICC imeshindwa kufanya uwekezaji katika Visiwa vya Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI):
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza kwamba Mheshimiwa Waziri wa Fedha alidanganya, naomba niseme siyo sahihi. Mheshimiwa Waziri wa Fedha hakudanganya, alisema Msajili wa Hazina wameunda mkakati kwa kushirikiana na kituo husika ili kuona kituo kinatoa gawio.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama amesikiliza vizuri katika jibu langu la msingi, nimesema kituo kimeanza kutoa gawio mwaka 2016/2017 na katika gawio hili Serikali ya Zanzibar inapata mgao wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili kwamba kituo hakiwekezi Zanzibar. Napenda kuliharifu Bunge lako tukufu kwamba kituo kinatekeleza mpango mkakati wa miaka mitano ambao umeanza kutekelezwa mwaka 2017/2018 hadi 2021/2022 na ambao katika mambo yanayotakiwa kutekelezwa ndani ya mpango mkakati huo ni kujenga vituo vingine kwa uwekezaji na katika maeneo ambayo vituo vitajengwa mojawapo ni Zanzibar na kituo kwa sasa kinaanza kujenga Dodoma na baada ya Dodoma kinakwenda kujenga Zanzibar. Kwa hiyo, uwekezaji huu unakwenda katika pande zote mbili za Muungano.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa gharama za maisha zimepanda na asilimia 10 ni sawa na milioni moja, sasa je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza kutoka asilimia 10 kwenda asilimia 50? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa Benki ya Wanawake iko Dar es Salaam tu, wanawake wa mikoa ya pembezoni wanaisikia tu hiyo benki. Je, ni lini Serikali sasa itafungua Tawi la Benki ya Wanawake Mkoa wa Rukwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swai lake la kwanza kuhusu kuongeza asilimia 10 hadi 50, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, Serikali yetu inatambua mchango wa wanawake katika kujenga uchumi wa Taifa letu. Hili ni pendekezo, tunalichukua kama Serikali. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kufuatia kuwatambua wanawake kwenye uchumi wa Taifa letu, ndiyo maana tulipopitisha bajeti ya TAMISEMI tuliondoa riba ambayo ilikuwa inachajiwa katika hii asilimia 10 ya mikopo waliyokuwa wanakopeshwa wanawake, hii ikiwa ni hatua ya kwanza kuhakikisha kuwa akina mama na vijana wanaendelea kupata mitaji inayopatikana na bila kurejesha kwa gharama nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, napenda kumwambia Mheshimiwa Bupe na Bunge lako tukufu kwamba Benki ya Wanawake Tanzania ilikumbwa na changamoto na sasa Serikali inaisimamia vizuri na tunatengeneza mfumo mzuri wa kuweza kufanya iweze kusimama. Moja ya mikakati ya kuiwezesha kusimama ni kupata mtaji wa kutosha, ndiyo maana kwa sasa kuna mapendekezo, wanafanya kazi kwa karibu na Benki yetu ya TPB na itakapoimarika ni nia ya Serikali kuona kwamba Benki ya Wanawake inaendelea kuwafikia wanawake kule walipo.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nina swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ieleweke kuwa Zanzibar hatupati gawio la Yeared Budget Support. Tunapata gawio la Annual Year Budget Support ambayo ni 4.5% na imekuwa ikishuka kila leo, nafahamu pia kuna vikao vingi vya harmonization vinavyoendelea. Sasa nilikuwa napenda tu Serikali ituambie wamefikia wapi juu ya kuweka mambo haya yote sawa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama swali lilivyojielekeza, liliuliza kuhusu Basket Fund ambao ndipo jibu langu la msingi lilipoeleza kulingana na sheria. Basket Fund ni kwa ajili ya Tanzania Bara kwa sababu na Zanzibar nao wanapata Basket Fund.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya General Budget Support, kama alivyouliza Mheshimiwa Khadija Nassir, napenda kulieleza Bunge lako tukufu kwamba kwa mwaka 2016/2017 General Budget Support iliyopelekwa Zanzibar ilikuwa ni shilingi 5,656,500,000 lakini pia kwa mwaka huu hadi Machi tayari Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeshapeleka shilingi 3,153,111,187.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto alizozisema Mheshimiwa Mbunge tunaendelea kuzishughulikia kwa pamoja tukifahamu umuhimu wa mapato kwa maendeleo ya Taifa letu.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Tunatambua baada ya Uchaguzi Mkuu uliopita baadhi ya nchi wafadhili zilizuia kutoa misaada yao kwa madai ya ukiukwaji wa uchaguzi wa Zanzibar na makosa ya mitandao hapa nchini. Serikali iliahidi kwamba mazungumzo yalikuwa yanaendelea ili kuhakikisha wafadhili wanaondoa vikwazo hivi. Nataka kujua je, mazungumzo yale yalifika wapi? Je, tumeanza kufaidika na misaada ile kutoka kwa nchi wafadhili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mazungumzo niliyosema yanaendelea sio kati ya Tanzania na nchi wahisani, hapana. Ni mazungumzo kati ya Serikali zetu mbili kuhusu hili. Sina uhakika sana kama kuna nchi zilizositisha misaada yao kwa sababu ya uchaguzi wa Zanzibar, hiyo siyo sahihi hata kidogo. Kitu ambacho kilikuwa kinasababisha mapato haya ya GBS yapungue ilikuwa ni kumalizika kwa muda wa mwongozo wa ushirikiano kati ya nchi yetu na nchi wahisani, ambapo napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba mwongozo mpya tayari umeshapatikana tangu Agosti, 2017 na tumeanza kuutumia kuanzia mwaka huu wa fedha. Kwa hiyo, mapato haya yanaendelea kupatikana.
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kanzidata zinatunzwa na hizi kampuni za simu na sio sisi wamiliki wa hizi kampuni na kwa kuwa inaweza ikatokea simu ikapotea au ikaibwa na kumbukumbu mtu asiwe nayo. Sasa je, Serikali iko tayari kupokea maelezo ambayo yatakuwa yameandikwa kwenye vocha ya malipo ambapo mfanyabiashara ameweka tu ile reference number, je Serikali itakuwa tayari kuikubali?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, tulivyoanzisha mifumo ya electronic devices (electronic signature device, electronic fiscal device na electronic tax register) wafanyabiashara wakubwa (large tax payers) walipewa bure kwa maana ya kwamba waliweza ku-claim kutoka kwenye uandaaji wa VAT return. Sasa kwa mpango huo ambao ulifanyika kwa wafanyabiashara wakubwa, je, Serikali haioni haja sasa ikatoa hizi EFD bure kwa wafanyabiashara wadogo au ikaweka ruzuku ambapo itawawezesha…
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwenye majibu yangu ya msingi nimesema kifungu cha 35(3) kinamtaka mlipa kodi mwenyewe kutunza kumbukumbu zake kwa miaka mitano mfululizo. Kifungu hiki kinaweka utaratibu wa kwamba unapokuja kukaguliwa na watu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania wanakutaka uwe na hizi kumbukumbu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe tu walipa kodi wetu wajitahidi kuwa na hizi kumbukumbu kama sheria inavyotuelekeza lakini kwa jitihada za Serikali yetu ya Awamu ya Tano makampuni yote ya simu yametakiwa kupitisha miamala yao katika kanzidata yetu pale Kinondoni. Kwa hiyo, kama mlipa kodi atakuwa amepoteza kumbukumbu zake ni rahisi zaidi kuzipata taarifa zake pale katika kituo chetu cha Kinondoni.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili, napenda kulihakikisha Bunge lako tukufu kwamba ni sahihi tuligawa mashine hizi kwa wafanyabiashara hasa kwa Mkoa wa Dar es Salaam na sasa tunaandaa utaratibu wa kuwafikia wafanyabishara wetu wote, lakini sio kwa kuwapa bure kwa sababu hata wale wa mwanzo hawakupewa bure, kilichofanyika anapewa mashine ya EFD halafu anakatwa kwenye kodi yake ambayo alitakiwa kuilipa Serikalini.
Mheshimiwa Spika, tunaendelea na mfumo huo na kuanzia tarehe 1 Julai, Mamlaka ya Mapato Tanzania itaanza yenyewe kugawa mashine hizi badala ya kutumia mawakala ambao wametuingiza gharama zisizo za msingi kwa wafanyabiashara wetu na tuna uhakika tunapolichukua jambo hili hata gharama za mashine hizi zitakuwa ndogo kwa wafanyabiashara wetu.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya majibu ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali ya nyongeza mawili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, makusanyo ya kodi za majengo katika Manispaa ya Iringa katika mwaka wa fedha 2015/2016, TRA iliweza kukusanya shilingi milioni 800. Katika upangaji wa bajeti wa Halmashauri ya Manispaa Iringa fedha za kodi ya majengo zilikuwa zimekadiriwa zisaidie miradi ya Manispaa ya Iringa. Hadi navyozungumza hapa hakuna hata senti tano iliyorudishwa. Je, nia ya Serikali ni kutaka kukwamisha maendeleo ya Manispaa ya Iringa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa vikao vya RCC. Halmashauri saba za Mkoa wa Iringa zilipeleka barua ya maombi maalum kama sheria inavyotaka, kuomba fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya. Wilaya ya Kilolo imefanikiwa kupewa shilingi bilioni moja na point, Wilaya ya Iringa vijiji imefanikiwa kupewa milioni moja na point, Wilaya ya Mufindi imefakiwa kupewa shilingi bilioni moja na point, Mafinga Mjini imefanikiwa kupewa shilingi milioni 400; Manispaa ya Iringa ilikuwa imeomba kibali maalum cha shilingi milioni 700, haikuweza kupewa fedha hizo. Je, fedha hizi zinalipwa kisiasa hasa ukizingatia Majimbo yaliyopewa fedha ni ya CCM na Jimbo la Manispaa ya Iringa ni la CHADEMA? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonukulima, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza, napenda kumwambia kwamba siyo nia ya Serikali kukwamisha maendeleo ya Halmashauri yoyote ile na ndiyo maana tarehe 5 Mei, 2018, Serikali imezindua Mpango Mkakati wa Kuziwesha Halmashauri kubuni miradi ya maendeleo itakayo-generate mapato kwa ajili ya Halmashauri husika na hatimaye kuhakikisha shughuli zote za maendeleo zinaendelea kutekelezwa ndani ya kila Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, napenda kwanza kumshukuru kwa kuweza kusema ndani ya Mkoa wa Iringa, Wilaya nne ndani ya miaka miwili ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli zimepewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya. Hilo ni jambo la msingi, naamini angetupongeza kama Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swaIi lake la pili amesema kwamba pesa zinatolewa kisiasa. Napenda kumwambia Mheshimiwa Mgonukulima kwamba Mheshimiwa Msigwa Mbunge wa Iringa Mjini yeye mwenyewe amekiri mbele ya Mheshimiwa Rais kwamba miradi mingi ya maendeleo inapelekwa kwenye Majimbo yote. Kwa hiyo, hakuna siasa kwenye utelekelezaji wa miradi ya maendeleo. (Makofi/Kicheko)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Serikali imechukua baadhi ya vyanzo vya mapato katika Halmashauri na kurudisha Serikali Kuu na vilevile imechukua baadhi ya watumishi kama watumishi wa Idara ya Ardhi na sasa watumishi wa Idara ya Maji. Je, Serikali haioni kwa kufanya hivyo inakwenda kinyume na sera yake ya D by D na mwisho wake ni kuziua kabisa hizi Halmashauri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la Mheshimiwa Selesini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, napenda kumwambia kwamba, uchukuaji wa vyanzo vile vya mapato ilikuwa kwa lengo moja na Bunge lako Tukufu liliridhia kwamba vichukuliwe ili ufanisi uonekane kwenye makusanyo na hatimaye fedha hizi ziweze kutekelezwa kulingana na bajeti za kila Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili la kuchukua watumishi, tuitendee haki Serikali yetu ya Awamu ya Tano, hakuna mtumishi aliyehamishwa kutoka Halmashauri moja kupelekwa kwenye Wizara yoyote. Watumishi wamebaki kwenye Halmashauri husika, lakini wanatakiwa kuripoti kwenye Wizara zao za kisekta. Kwa hiyo, hakuna mtumishi yeyote aliyeondolewa ndani ya Halmashauri. Tunachokifanya kama Serikali ni kuboresha tu utendaji kazi wa watumishi hawa kwa manufaa mapana ya Taifa letu wananchi wetu kwa ujumla.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Ngara ni miongoni mwa Halmashauri ambazo ziliendelea kuruhusiwa kukusanya kodi ya majengo lakini Mkurugenzi wa Halmashauri yangu ya Wilaya ya Ngara amekuwa akienda tofauti na kinyume na kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana ilielekezwa kwamba majengo yote itakuwa ni flat rate Sh.10,000, ghorofa Sh.50,000 kwa floor, lakini katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Rulenge sasa hivi kuna mtafaruku mkubwa, nyumba ambazo hazijakamilika…

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi kuna nyumba za tope zinatozwa kodi, kuna nyumba za wazee wa zaidi ya miaka 70 zinatozwa Sh.200,000 mpaka Sh.300,000. Naomba Serikali itoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ngara kwa sababu ni usumbufu na anawatishia kwamba atawapeleka Mahakamani wakati anakiuka sheria na kanuni ya makusanyo ya fedha hizo za property tax. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la Mheshimiwa Gashaza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa maelekezo ya Serikali na sheria iliyopitishwa na Bunge lako Tukufu ilikuwa kwamba majengo yote ambayo hayajafanyiwa tathmini yatatozwa flat rate ya Sh.10,000 kwa majengo ya kawaida na kila ghorofa litatozwa Sh.50,000, kama tu halijafanyiwa tathmini. Kwa majengo yanayotozwa zaidi ya pesa hiyo ni majengo yaliyofanyiwa tathmini, ndiyo sheria iliyopitishwa na Bunge lako Tukufu inavyosema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri tajwa kwamba kama anakwenda kinyume na hivyo, anatakiwa kuwashirikisha wananchi wake kwamba tathmini imeshafanyika na kinachotozwa ni kodi stahiki. Kama tathmini haijafanyika, hatakiwi kutoza kodi hiyo anayoitoza. Pia sheria iliyopitishwa na Bunge lako Tukufu, iliainisha ni nyumba za aina gani. Kwa hiyo, namwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri husika aweze kufuata sheria na taratibu.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali inapeleka fedha Halmashauri kulingana na makusanyo lakini kumekuwepo na malimbikizo ya madeni yanayotokana na stahiki za watumishi kama gharama za mazishi, matibabu yasiyo ya Bima za Afya, gharama za kufungasha mizigo kwa wastaafu, masomo na likizo. Je, ni lini Serikali italipa madeni ya mwaka 2016/2017 yaliyohakikiwa na kuwasilishwa Januari, 2018? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali ilipunguza ruzuku ya matumizi ya kawaida kutoka asilimia 100 kwenda asilimia 40, mafungu niliyoyataja yanaonekana kuelemewa. Je, Serikali haioni ipo haja ya kufanya mapitio katika mafungu niliyoyataja na kuweza kuyaongezea bajeti? Mheshimiwa Spika, ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Leah Komanya, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la kwanza la kulipa madeni ambayo yameshahakikiwa, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu imekuwa ikilipa madeni yote ambayo yamehakikiwa kwa ajili ya watumishi wetu. Kama ambavyo nimekuwa nikiliarifu Bunge lako Tukufu ni mwezi Aprili tu Serikali yetu ililipa zaidi ya shilingi bilioni 43 kwa ajili ya madai mbalimbali ya watumishi wetu katika Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Spika, kuhusu kuongezewa kwa bajeti katika mafungu aliyoyataja Mheshimiwa Leah Komanya, napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba katika mafungu ambayo tunayapa kipaumbele kuyapatia fedha za ruzuku ni Mafungu ya Utawala ambayo ndiyo yanashughulikia haya matatizo aliyoyasema kama gharama za mazishi na gharama za uhamisho. Kwa mfano, kwa mwaka huu 2017/2018 tuliomaliza tulikuwa na bajeti ya Sh.27,447,000,000. Kati ya hizi shilingi bilioni 27, Serikali yetu ilipeleka shilingi bilioni 22 kulingana na mahitaji yaliyoletwa kutoka kwenye Halmashauri zetu ambayo ni zaidi ya asilimia 90 ya bajeti ambayo ilikuwa imepangwa. Hili lilikuwa ni Fungu la Utawala ambalo ndilo linaloshughulika na madai mbalimbali aliyoyataja Mheshimiwa Leah Komanya.
Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine ambayo tunatoa kipaumbele kupeleka fedha za ruzuku ni katika Fungu la Elimu ambapo Serikali yetu imekuwa ikiajiri Walimu na tunahakikisha Walimu wetu wanalipwa pesa zao kabla hawajafika kwenye vituo vyao vya kazi au wanapofika tu kwenye vituo vyao vya kazi. Kwa mfano, kwa mwaka 2017/ 2018 tulipanga kupeleka shilingi bilioni 116 na tukapeleka zaidi ya shilingi bilioni 111 kulingana na mahitaji yaliyoletwa kutoka kwenye Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba tunajua umuhimu wa mafungu haya na tunayapa kipaumbele katika kuyapelekea fedha za ruzuku.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Spika, naomba kwa ruhusa yako kabla sijauliza maswali yangu mawili madogo ya nyongeza, kwanza niwashukuru timu ya kampeni iliyotoka Kakonko, uniruhusu niwapongeze Wabunge wote wa CCM na Upinzani waliokuja Kakonko kwa kampeni. Tunasema tunashukuru sana kwa changamoto mlizotupa na tunaendelea kumpongeza Mheshimiwa Chiza kwa ushindi mnono alioupata. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya maneno machache ya utangulizi, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, msingi wa swali langu ni mikoa ile mitano ambayo iko nyuma, ndiyo msingi wa hoja na si suala la Ilani ya Uchaguzi ya CCM, si suala la Mpango wa Miaka Mitano. Hoja ni mikoa mitano iliyoko nyuma ambayo inahitaji kupata special attention, inahitaji equalization ili iweze kulingana na mikoa mingine ndiyo msingi wa swali.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza la nyongeza ni kwamba miradi yote aliyoitaja ukiacha ujenzi wa reli ya kati, hiyo miradi haijatekelezwa na mingine ina miaka 20. Hiyo mikoa mitano iliyoko nyuma inahitaji kubebwa, kusaidiwa itoke katika maeneo yale ili iweze kuwa sawa sawa na mikoa mingine. Je, ni nini mkakati wa Serikali kwa mikoa hii?
Mheshimiwa Spika, swali la pili la nyongeza ni kwamba hiki kinachoitwa North-West Grid, ni mradi ambao una urefu wa kilometa 2,500 kutoka Tunduma – Nyakanazi kupitia Sumbawanga – Mpanda – Kigoma – Kasulu – Kibondo mpaka Nyakanazi. Je, mradi huu utakapoanza kutekelezwa kwa nini usiwe na wakandarasi zaidi ya watatu ili uishe kwa haraka ili wananchi tupate umeme katika maeneo haya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Daniel Nsanzugwanko, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza amesema msingi wa swali lake ni mikoa mitano maskini, lakini alikwenda specific na kuutaja Mkoa wa Kigoma na ndiyo maana na mimi nilijibu specifically kwa Mkoa wa Kigoma, nini ambacho Serikali yetu inafanya.
Mheshimiwa Spika, napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba kupitia miradi ya maendeleo kama nilivyoitaja ndiyo fursa a kiuchumi hufunguliwa kwa ajili ya wananchi wetu kwenye mikoa husika. Kupitia Mpango wa Pili wa Maendeleo, mpango wa maendeleo wa mwaka mmoja mmoja, Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ndiko vipaumbele huwekwa kulingana na geographical location ya mikoa yetu na aina ya umaskini. Kwa hiyo, miradi hupangwa kulingana na miongozo hiyo niliyoitaja. Kwa hiyo, naomba tu Mheshimiwa Daniel akubaliane na jibu hili kwamba hatuwezi kupanga bajeti nje ya miongozo na mipango inayotuongoza.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili ametoa pendekezo, tutakaa kama Serikali na Wizara ya Nishati kuona jinsi gani mradi huu wa North – West Grid utatekelezwa kwa haraka ili kurahisisha maendeleo ambayo tunayataka yafike kwa wananchi wetu.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nimkumbushe tu kidogo Mheshimiwa Naibu Waziri kwa vile alikuwa ni mwalimu wangu kullu-kum rai, wakullu-kum mas-ul alayhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, waliokuwa wafanyakazi wa benki ambayo waliondolewa kazini na wasimamizi wa Deposit Insurance Board (DIB) ndio wakasimamia ufilisi wa benki hiyo. Hawajalipa wafanyakazi hao mpaka sasa hivi na ukizingatia ni wapiga kura wetu, ni wananchi wetu kwa muda mrefu sasa hivi. Je, haioni sheria hiyo aliyoitaja kuwa imepitwa na wakati na inawakandamiza wananchi na lini ataleta sheria hiyo? That is (a).
Mheshimiwa Mwenyekiti, ya pili katika majibu yake alisema kukusanya madeni pamoja na fedha za benki zilizopo kwenye benki nyingine nje ya nchi na kulipa amana za benki, nataka nimwambie tu FBME correspondence bank ni Dutch Bank hebu tuambie kiasi gani ambazo ziko huko na lini zitaletwa ili wananchi hao na Serikali kukosa mapato. Na hivi juzi tumeshuhudia makontena kupigwa mnada wananchi wanataka kununua makontena hayo ili wapate biashara?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza ni swali la wafanyakazi wa iliyokuwa Benki ya FBME. Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba, taratibu za wafanyakazi zinashughulikiwa na sheria za kazi za Taifa letu. Kwa hiyo, wafanyakazi wale walipoajiriwa na benki hii walisaini mikataba na hivyo sheria za kazi za Taifa letu zinaendelea kusimamia haki ya wafanyakazi wote waliokuwa wa benki hii ya FBME.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili napenda kumwambia Mheshimiwa Jaku Hashim kwamba avute subira tunaendelea kufuatilia kama anavyofahamu yeye kwamba benki hii ilikuwa ni benki ambayo asilimia 10 ya uendeshaji wake ulikuwa ndani ya Taifa letu na asilimia 90 ulikuwa nchini Cyprus. Kama Wizara na Benki Kuu tunaendelea kulifuatilia jambo hili kwa ukaribu na tunawahakikishia wateja wetu watapata fedha zao kwa muda muafaka.
MHE. MUSSA B. MBAROUK: Mheshimiwa Spika, ndiyo, maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, risiti ni supporting document katika masuala ya mahesabu. Sasa risiti zetu za EFD machines zina tabia ya kufutika maandishi baada ya muda mfupi, TRA tulipokutana nao katika Kamati yetu ya PAC walikiri kwanza kwamba karatasi wanazotumia ni dhaifu lakini wakasema kwamba watafanya marekebisho ya karatasi hizo ili zisifutike maandishi kwa muda mfupi. Mpaka leo, tarehe 10 Septemba, bado marekebisho hayo hayajafanyika.
Mheshimiwa Spika, nataka kujua sasa TRA tuipe muda gani ili iweze kufanya marekebisho ya karatasi hizi za risiti?
Pili, mwaka 2017 mwanzoni wafanyabiashara wa Mkoa wa Mbeya waligoma baada ya baadhi yao kwenda China na kubaini kwamba mashine zile gharama yake ni sawasawa na shilingi 90,000 ya Kitanzania kwa mujibu wa vyombo vya habari vilivyoripoti wakati ule. Sasa nataka kujua, je, hizi mashine bei yake halisi hasa na taarifa hizi zina ukweli kiasi gani?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza kuhusu karatasi zinazofutika, napenda kuliambia Bunge lako tukufu kwamba Serikali ilishatoa taarifa kwa wafanyabiashara wote kuhusu wapi pa kununua karatasi hizi kwa ajili ya kutoa risiti za mashine za EFD. Zipo karatasi fake, hatukatai, zipo sokoni, lakini tumewaelekeza wafanyabiashara wote waende kununua karatasi hizi kutoka kwa mawakala waliothibitishwa na kuidhinishwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania ili kuepuka tatizo hili la karatasi kufutika.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, anasema wawape muda mpaka lini, hatuhitaji kupewa muda kwa sababu tatizo hili tulishalishughulikia tayari kama Serikali.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili; nashukuru umenisaidia kumjibu kwamba gharama za mashine ndizo nilizozitaja hapa kulingana na aina ya mashine na aina ya biashara mfanyabiashara anayoifanya. Kwa hiyo, hizo nyingine za kwenye vyombo vya habari, hizo kama Serikali hatuzijui, tunazojua ni hizi nilizozisema, ndiyo kauli na taarifa sahihi kutoka Serikalini. (Makofi)
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na maswali mawili ya nyongeza.
Je, Serikali inatumia vigezo gani kwa wananchi kupata hiyo mikopo?
Swali la pili, atakubaliana na mimi Mheshimiwa Naibu Waziri akiongozana na watalaam wake waende Jimboni kwangu kwenda kutoa elimu na kwa sababu wananchi wanataka kukopa fedha hizi ili wananchi na wao waondokane na umaskini. Je, Serikali lini watakwenda Jimboni kwangu Bububu ili kwenda kutoa mikopo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lako la kwanza kuhusu vigezo, kigezo kikubwa ambacho benki yetu ya kilimo inaangalia ili iweze kumkopesha mkulima ni kuangalia kama mradi ule unaotekelezwa na mkulima unaweza kukopesheka yaani valuable agricultural activity ambayo inaweza akawekeza na akapata faida yake na akaweza kurejesha mkopo huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakatika hili ndio maana Benki Kuu imetoa maelekezo kwa mabenki yetu yote kuhakikisha kwamba wakopeshwaji ambao wanaomba mikopo wanakuwa ni wale ambao taarifa zao zinaonesha wameweza kukopa na wakarejesha mikopo ili kuondokana na tatizo la mikopo chechefu ambayo mabenki yetu mengi yanapambana nayo. Serikali yetu ya Awamu ya Tano imepanga kuhakikisha wakulima wetu wanafikiwa na mikopo hii ya benki ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, namuahidi Mheshimiwa Mwantakaje baada ya Bunge hili mimi na watalaam wangu wa Benki yetu ya Kilimo tutakuja Jimboni kwako Bububu kuja kuwatembelea wakulima wa Bububu. (Makofi)
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mheshimiwa Waziri naomba unisikilize kwa makini swali langu likukune mithili ya nazi na unipe jibu mfano wa tui. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, nakubaliana na maelezo uliyoyatoa juu ya uanishaji wa kukua kwa uchumi wa nchi. Mheshimiwa Waziri lakini katika kipindi hiki ambacho tunashuhudia pato la Taifa likiwa limesimama la dola 976 mpaka mwaka 2016, tunashuhudia upungufu wa uuzaji wa bidhaa nje ya nchi, tunashuhudia bei za huduma zikitetereka mfano majengo ambapo sasa hivi yanakosa wapangaji, tunashuhudia fedha yetu ikiendelea kushuka… (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, kuna uhusiano gani wowote ambao unaonesha kweli hali ya uchumi inakua wakati hali ya wananchi kukosa pesa inazidi kuongezeka miongoni mwetu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, nchi za kiafrika zimeingia katika mtego au mahusiano na China inayosababisha wote kukimbilia kukopa China. Jambo hili linasababisha wanaposhindwa kurejesha mikopo kukamatiwa mali zao na tayari baadhi ya nchi jirani zimeanza kukamatiwa mali zao na kudhibitiwa na China. Je, mnachukua tahadhari gani kwa nchi yetu kuja kutumbukia katika mfumo huo wa kuja kukamatiwa nchi yetu na ikawa koloni la China? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khatib Said Haji, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimwambie pato la Taifa halijasimama wala halijashuka. Tumeendelea kuleta taarifa sahihi ndani ya Bunge lako Tukufu kuhusu ukuaji wa uchumi wa Taifa letu, tumeonyesha jinsi gani unakua na nimeonyesha vigezo hivi na kitakwimu Mheshimiwa Khatib tuwasiliane ili nikupatie takwimu ujue taifa letu linakwenda wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza amezungumzia wananchi kukosa pesa, naomba nimwambie Mheshimiwa Khatib na Bunge lako Tukufu kwamba money supply kwenye uchumi siyo kigezo cha kukua kwa uchumi wa Taifa. Money supply kwenye uchumi inaonesha kwamba Taifa hilo limeshindwa ku-control ukuaji wa uchumi wake. In short run inaweza ukajidanganya ukuaji wa uchumi upo lakini in long run matatizo na madhara yake ni makubwa sana. Nimpongeze sana Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania pamoja na wataalam wake wanafanya kazi kubwa kuhakikisha hakuna pesa za ziada kwenye uchumi wetu ili tusiingie kwenye matatizo makubwa ya kiuchumi, hilo ni jibu la kwanza kwa swali la Mheshimiwa Khatib. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lako la pili, hizi ni speculative ambazo zipo kwenye vyombo vya habari. Napenda kumwambia kwamba kwa Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tupo makini sana wapi tunakwenda kukopa, kwa riba ya kiasi gani na kwa nini tunakwenda kukopa. Ndiyo maana sasa hivi Bunge lako Tukufu linajadili Muswada wa Sheria ya Ubia kati ya Sekta Binafsi na Sekta ya Umma, ni umakini ule ule wa Serikali yetu ya Awamu ya Tano kuhakikisha Taifa letu linakwenda kuwa salama. (Makofi)
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri bado anaona kwamba uchumi unakua wakati masoko ya wananchi ya mazao yao hayapo, hakuna annual increment kwa wafanyakazi, hakuna mazingira mazuri ya wafanyabiashara wetu kufanya biashara jambo ambalo limesababisha stress kwa wananchi na tumeshuhudia matukio ya watoto kuchomwa moto kwa upotevu wa Sh.2,000 na mwanafunzi kuuawa kwa sababu ya Sh.75,000…
Kwa nini bado anaona uchumi unakua wakati stress hizi zimesababisha matukio makubwa katika Taifa letu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gekul, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini naamini uchumi wa Taifa unakua ni kwa sababu ya takwimu na hali halisi ya uchumi wetu ulivyo.
Napenda kuliambia Bunge lako tukufu na uniruhusu nisome kipengele hiki kwenye mkutano uliokwisha mwezi uliopita wa Wakuu wa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara (SADC) yalisemwa haya yafuatayo kuhusu uchumi wa Taifa letu, naomba kusoma, mkutano uliombwa ku-note that the majority of member states underperformed in achieving the agreed microeconomic indicators only three member states of SADC have attained that and all these three countries is Botswana, Lesotho and Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa Taifa letu unakua, watu wa nje wanaona kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Watanzania wanayaona na tupo imara tutaendelea kusimamia uchumi wa Taifa letu. (Makofi)
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti ya CAG iliyoishia Juni, 2017 imeonesha kwamba katika kaguzi zilizofanywa hasa katika Shirika la RAHCO ilitumia shilingi bilioni 20 kufanya upembuzi yakinifu wa miradi minne, lakini shilingi bilioni 20 zimepotea kutokana na kwamba miradi hiyo haikutekelezwa au haitekelezeki.
Je, Mheshimiwa Waziri atakubaliana nami kwamba kuna harufu ya ufisadi katika miradi hii minne ambayo ametumia shilingi bilioni 20 wakati ikijulikana miradi hii haiwezi kufanyika? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, imeonekana Wabunge wengi walikuwa wamelalamikia miradi ambayo inafanywa chini ya viwango ikitekelezwa na Wizara za Maji na Wizara za Ujenzi hasa TANROADS na kwamba pesa nyingi inatumika kwenye upembuzi yakinifu lakini nakuta miradi hiyo haifanywi.
Je, Serikali inakubaliana nami kwamba kuna sababu ya kumwomba Mheshimiwa Spika aunde Tume ya Kibunge ambayo itachunguza haya yote kwamba inakuwaje ifanywe miradi ya upembuzi yakinifu, lakini miradi hiyo haitengewi hela mwaka hadi mwaka? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza kwamba kwenye upembuzi yakinifu wa NAFCO kwamba kulikuwa na ufisadi. Kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi ni kwamba hizi ni taarifa za kisekta na zinafanyiwa kazi na Wizara husika za kisekta. Inakuwa ni ngumu kwa mimi kusema kulikuwa na harufu ya ufisadi kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge amelitamka hili ndani ya Bunge lako tukufu; Serikali yetu ni moja, tunalifanyia kazi kuona jambo hili linafanyiwa kazi kabla ya kukiri aidha kulikuwa na ufisadi au hakukuwa na ufisadi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, nimesema kwenye jibu langu la msingi Serikali yetu hufuata Katiba, Sheria, Kanuni zikiwemo Kanuni za Bunge lako tukufu na hivyo Serikali haina mamlaka ya kulipangia Bunge nini cha kufanya. Kama Bunge lako tukufu litajiridhisha kuna umuhimu wa kuunda Tume kwa ajili ya kazi hiyo anayopendekeza Mheshimiwa Mbunge, Serikali yetu iko tayari kabisa kuona hilo linatekelezwa kwa sababu ni majukumu ya Bunge kusimamia Serikali yetu. Ahsante.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Serikali wakati ikitoa ufafanuzi kuhusiana na kukosekana kwa taarifa za matumizi ya shilingi trilioni 1.5 ilielezwa kwamba kati ya fedha zile shilingi bilioni 200 ni makusanyo ya Zanzibar.
Sasa Mheshimiwa Waziri kabla nazo hazijatumbukia katika kero ya Muungano ni lini fedha hizi zitafika Zanzibar? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili liliulizwa wakati tukijadili bajeti ya Wizara yetu ya Fedha na Mipango na sisi kama Serikali tuliacha kulijibu makusudi kwa sababu tunafahamu mchakato wa kujadili hoja hizi za CAG ukoje, itakapokwenda kwenye Kamati ya PAC tukija hapa itajadiliwa kwa kina. Hata hivyo, naomba kusema yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi bilioni 203 ni fedha inayokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania Zanzibar na huwa hazivuki maji kuja Tanzania Bara. Zinakusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania na kuingia moja kwa moja kwenye akaunti.
Naomba msikilize basi niwape elimu ili tuweze kuelewana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizo hukusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania inayofanya kazi zake Zanzibar; na zinapokusanywa fedha hizo zinasomeka kwenye financial statement za Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa sababu zinakusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania. Fedha hizo hazivuki maji kuja Tanzania Bara, huingia moja kwa moja kwenye akaunti kuu ya Pay Master General Zanzibar. Kwa hiyo, fedha hizo zimekwenda moja kwa moja kwenye akaunti ya Mlipaji Mkuu wa Serikali ya Zanzibar. (Makofi)
MHE. MASOUD A. SALIM: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nionyeshe masikitiko yangu na mkanganyiko wa majibu ya taarifa zao mbalimbali za hali ya uchumi pamoja na utaalam wao wakitoa shule hapa Bungeni.
Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza, Deni la Taifa linaongezeka na mnaendelea kukopa madeni ya masharti ya kibiashara ambayo yanapelekea sisi Watanzania kupata matatizo makubwa wakati mkiandaa mazingira ya kutaka kulipa deni hilo nje au kama inavyotakiwa. Ukiangalia taarifa nyingine zinaeleza kwamba bado mna mpango wa kukopa Sh.4,840,000,000 kwa ajili ya kulipa Deni hilo la Taifa. Je, kwa hali hii ya uchumi ilivyo na mkakati huo wa kulipa Deni la Taifa mtahimili kweli au mnataka mnataka nchi iendelee kufilisika?
Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kwamba Deni la Taifa halijafanyiwa uhakiki (credit rating) ili nchi yetu iweze kujiridhisha kwamba Serikali inakopesheka au haikopesheki. Naomba atuambie ni lini mkakati huo ufanyika haraka ili nchi yetu ifanyiwe credit rating hali iwe nzuri kama ambavyo inavyoendelea katika nchi nyingine?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali ya Mheshimiwa Masoud Abdallah, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza kuhusu mkakati wa kulipa na kama deni letu ni stahimilivu, naomba nimwambie, kwanza Serikali yetu haijawahi ku-default hata mwezi mmoja katika kulipa madeni ambayo yameiva kwenye taasisi zote ambazo tumekopa. Ndiyo maana bado Taifa letu limeendelea kuaminiwa na taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa na tunaendelea kukopa kwa uangalifu wa hali ya juu. Tunapokopa tunahakikisha mikopo yote tunayoikopa tunapeleka katika shughuli za maendeleo ya kiuchumi, ambapo tutaendelea kunyanyua uchumi wa Taifa letu na hasa tunapotelekeza azimio hili la Mheshimiwa Rais wetu la Tanzania ya Viwanda ambapo mpaka mwaka 2025 kwa uchumi wetu unavyokuwa tuna uhakika Taifa letu litakuwa ni Taifa la pato la uchumi wa kati. Napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba, kwa viashiria vyote kuhusu ukopaji na kulipa bado Taifa letu deni lake ni himilivu.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu credit rating, kama nilivyosema wakati tuna-conclude bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango kwamba mkataba ule upo ndani ya Ofisi ya AG na anaendelea kuufanyia rating ya mwisho. Tuna uhakika ndani ya mwaka ujao wa fedha Taifa letu litafanyiwa credit rating ili kujua sawasawa na mataifa yote duniani yaweze kufahamu kwamba Tanzania ni Taifa makini linaloaminiwa kiuchumi ndani na nje ya Taifa letu.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swali langu linamuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha, je, ni lini Bunge pamoja na Wizara ya Fedha wataleta Muswada mpya wa kuweza kuidhibiti Serikali kukopa madeni kwa maana imeonekana tuna madeni makubwa na Serikali inakopa bila ya sisi Wabunge kufahamu?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali moja la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali yetu ya Awamu ya Tano, kama ambavyo nimekuwa nikiliambia Bunge lako Tukufu tunafuata sheria, Katiba na taratibu zote za Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu ukopaji Serikali yetu imeendelea kusimamia Deni la Taifa kwa kuzingatia Sheria ya Mikopo, Dhamana na Misaada, Sura 134. Hakuna hata siku moja ambapo Serikali yetu imekopa bila Bunge lako Tukufu kujulishwa na kupitisha. Huwa tunaleta tunavyoleta bajeti ya Serikali tunataraji kukopa kiasi gani, Bunge lako linaturuhusu na tunakwenda kukopa kile tulichoruhusiwa na Bunge lako Tukufu.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kumekuwa na mkanganyiko mkubwa sana katika Deni hili la Taifa, Wabunge wamekuwa wakihoji sana kwamba deni limekuwa kubwa na wanahoji pia kwamba Serikali imekuwa ikikopa fedha na kulipia kwenye madeni ambayo tumekopa katika maeneo mengine. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuleta sheria ndani ya Bunge ili fedha yoyote inayokopwa na Serikali itakiwe kuidhinishwa ndani ya Bunge kwamba sasa Serikali ikope? Siyo Serikali inakopa tu halafu baadaye kunakuwa na hoja ambazo zinaleta mkanganyiko ndani Bunge hili na kwa Watanzania pia wanashindwa kujua fedha hizi zimefanya kazi gani. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Frank, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kama nilivyomjibu Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Serikali hukopa baada ya Bunge lako Tukufu kupitisha kiwango kilichoombwa na Serikali kuhusu ukopaji huo na nimetaja sheria inayosimamia haya yote tunayoyatenda. Napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba katika kipindi ambacho Serikali yetu ilitakiwa kupongezwa ni kipindi cha Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa sababu tumeimarisha makusanyo ya mapato yetu ya ndani na tunalipa deni letu kupitia makusanyo ya mapato yetu ya ndani.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Spika, ahsante. Zanzibar ni Kisiwa kidogo chenye wakazi wachache sana, wakazi wa Zanzibar ni kati ya 1,000,000 mpaka 1,500,000 na kutokana na hali hiyo Zanzibar inategemea soko la bidhaa kutoka nje. Maana yake Zanzibar inategemea soko la bidhaa zinazotoka nje kusafirishwa nchi jirani au baadhi ya nchi nyingine ili kutafuta soko na ndiyo maana Zanzibar imejiandalia mfumo wake mahsusi ili kufanikisha wafanyabiashara kutoka nchi nyingine ikiwemo Tanzania Bara wafike Zanzibar wachukue bidhaa zinazotoka nje kwa ajili ya kwenda kufanya biashara sehemu nyingine.
Mheshimiwa Spika, sasa Serikali haioni kwamba kuilazimisha Zanzibar kufata mfumo wa TANCIS ndiyo maana ya kuua soko la bidhaa kutoka nje kwa pale Visiwa vya Zanzibar? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Waziri kasema haiwezekani kuunda Tume, Bunge haliwezi kuunda Tume. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, Je, Serikali kupitia Wizara ya Fedha ipo tayari kuunda Kamati Ndogo wakiwemo Wabunge, Maafisa wa TRA na yeye mwenyewe kwenda Zanzibar kukutana na wadau, wafanyabiashara wa Zanzibar hususan Taasisi ya Wafanyabishara Zanzibar ili kuangalia ukubwa wa tatizo hili na kulitafutia ufumbuzi? Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi ni kwamba hiki kinachotokea ni kuhakikisha kunakuwa na ushindani katika soko la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ndiyo maana bidhaa zinazouzwa kutoka Zanzibar zilizotoka nje kuja Tanzania Bara lazima zifanyiwe uthamini ili kuhakikisha wafanyabiashara wanaotumia Bandari za Serikali ya Jamhuri ya Tanzania Bara wanapata ushindani ulio sawia.
Mheshimiwa Spika, amesema kwamba wafanyabiashara kutoka nchi nyingine. Kumekuwa na tatizo la wafanyabiashara kutoka nchi nyingine kwenda kununua bidhaa Zanzibar na kuja kuzi-dump katika soko la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ndiyo maana kwa sababu bidhaa zile hazijazalishwa Zanzibar lazima zinapoingia Tanzania Bara ziweze kulipa kodi husika ili ushindani huo uweze kuwepo.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, napenda kumwambia Mheshimiwa Kombo kwamba nimesema kwenye jibu langu la msingi Serikali zetu mbili, Serikali ya Zanzibar pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinalifanyia kazi tatizo hili na tuna uhakika kwamba changamoto hii itafika mwisho, kwa sababu majadiliano yamefika sehemu nzuri na tuna imani kubwa kwamba changamoto hii itafika mwisho sasa.

MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona. Ni lini Serikali italeta marekebisho ya Sheria Bungeni ili umeme unaonunuliwa Tanzania Bara kwenda Zanzibar uweze kupatiwa msamaha wa kodi kama ilivyo bidhaa nyingine zinazozalishwa Tanzania Bara kwenda Zanzibar? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, wakati tunapitisha Bajeti ya Wizara ya Nishati, Waziri wa Nishati alisema vizuri kabisa kuhusu jambo hili, kwamba nalo ni katika mambo ambayo yapo katika mijadala kuhakikisha kwamba kodi inayotozwa kwa umeme unaouzwa Zanzibar inafanyiwa kazi. Nimwombe Mheshimiwa Khadija Nassir pamoja na Wazanzibari wote na Watanzania wote jambo hili litafanyiwa kazi kwa muda muafaka kabisa.
MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwenye jibu lake la msingi kwamba watumishi wanapaswa kulipwa mafao yao hata kama hawakuwa wanakatwa, lakini hilo halifanyiki. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba hawa watumishi wanapata mafao yao? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa watumishi wastaafu wanapata pensheni yao ndogo sana, kuna watumishi wanapata Sh.50,000 kwa mwezi, kwa kweli kiasi hicho ni kidogo sana. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha inaongeza kiasi hicho cha pensheni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kumwambia Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba hili jambo analosema halifanyiki, siyo sahihi. Kwa sababu watumishi wote ambao waliajiriwa na walikuwa hawachangii kabla ya Mfuko wa Pensheni wa PSPF kuanzishwa walikuwa wakilipwa na Serikali Kuu kupitia Hazina. Kwa sasa kile kilichokuwa kinalipwa kupitia Hazina ndicho kimeunganishwa na malipo yao ya PSPF na wanalipwa pensheni yao yote kama ambavyo wanastahili kulipwa.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, sina uhakika sana labda nikae na Mheshimiwa Mbunge ni wastaafu gani wanaolipwa pensheni ya Sh.50,000, kwa sababu Serikali iliongeza pensheni ambayo ni kiwango cha chini kutoka Sh.50,000 kwenda Sh.100,000 na Mifuko yote ya Hifadhi ya Jamii inalipa Sh.100,000 kwa watumishi wote kama kiwango cha chini. (Makofi)
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ukiacha waaguzi lakini pia wafanyakazi wengi wa Idara zingine Serikalini wanacheleweshewa sana mafao. Mfano ni Askari Magereza wanastaafu lakini wanakaa zaidi ya miaka miwili hawajaenda kwao. Wanaganda kwenye zile kota za Magereza lane, mafao hamna, mtu kastaafu miaka miwili anadhalilika kwao Tanga, kwao Kilimanjaro, kwao wapi, hawezi kwenda kwa sababu hajapewa mafao yao wala pensheni.
Mheshimiwa Spika, sasa hii Serikali inawaangalia kwa jicho lipi hawa Askari Magereza kwa sababu, wao wamezoea kuwa-support Polisi ambao wanatukamata, lakini wahalifu wako maeneo mbalimbali, wanakusanywa yale maeneo mbalimbali, wanapelekwa eneo moja ambalo ni Magereza. Wale jamaa wana kazi ngumu sana kuwatunza mle, lakini wanafanya utumishi wao, wanakuja wanastaafu, mtu anakaa Police Lane miaka miwili hajapewa pension wala mafao yake, kwa nini wanawafanyia hivi Askari Magereza? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ameuliza, kuhusu mkakati wa Serikali yetu, naomba nimwambie Mheshimiwa Mbilinyi, mkakati wa kwanza wa Serikali yetu ilikuwa ni kulipa madeni yote ya michango ya mwajiri ambayo Serikali ilikuwa ikidaiwa na mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Napenda kumwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba, mpaka leo ninapoongea madeni yote yaliyokuwa yanadaiwa ya michango Serikali yetu ya Awamu ya Tano tayari imeshalipa zaidi ya shilingi bilioni 282 ili kuhakikisha wastaafu wetu wanalipwa mafao yao kwa muda muafaka.
Mheshimiwa Spika, mkakati wa pili, ilikuwa ni kuona jinsi gani ya kuunganisha Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii, ili pesa zilizopo ziweze kutumika inavyotakiwa na kuwanufaisha wastaafu wetu pale wanapostaafu. Namwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba, Julai Mosi, mifuko yote imeshaunganishwa na sasa tuna mifuko miwili, tatizo hili litaondoka bila wasiwasi wowote.
MHE. RASHID ALI ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili ni la muda mrefu sana kabla hata dhana ya kuunganisha Mifuko ilikuwa haijafikiwa, ndiyo linakuja leo. Pamoja na mambo hayo nitakuwa na swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, deni la trilioni 2.1 ndani yake kuna malimbikizo makubwa ya riba ambayo yamesababishwa na Serikali kwa kutokulipa kwa muda mrefu. Mifuko bado haijaunganishwa lakini riba haisubiri Mifuko kuunganishwa inaendelea. Ni hatua gani Serikali inachukua kuhakikisha kwamba Mifuko hii inaunganishwa haraka ili kunusuru riba hii isiongezeke? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba sheria tayari imeshasainiwa na Mheshimiwa Rais na kanuni zimeshakamilika. Ndani ya mwezi huu wa Tano Serikali inazipeleka kanuni kwa wadau ili tuweze kupata maoni yao na sisi kama Serikali tunatambua umuhimu wa kuiwezesha Mifuko kwa madeni yao haya, tuko tayari kulipa pale kanuni zitakapokuwa zimekamilika. Ahsante.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza katika hili napenda kwa dhati kabisa kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi zake katika kuhakikisha benki zinaendelea kupunguza riba za mikopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ni kweli benki zimeanza kuitikia wito huu na kipekee niipongeze Benki ya CRDB kwa kuwa wa kwanza kuitikia wito huu. Hata hivyo, inaonekana mikopo ambayo inapewa unafuu wa riba na kwa haraka ni ya wafanyakazi na watumishi wa umma lakini mikopo ya kibiashara bado mabenki yanaonekana kusuasua katika kufikia lengo hilo. Je, Serikali inatoa kauli gani ya kuzitaka benki kushusha riba kwa mikopo ya kibiashara?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mara nyingi tu katika Bunge hili nimekuwa nikisema kwamba kiwango kikubwa cha riba katika benki kinatokana na kiwango cha T-Bills ambacho kinapangwa na Serikali BOT. Je, Serikali inatoa kauli gani kuwa riba zinazotozwa na microfinances ambazo ndiyo kimbilio kubwa la wananchi wa kawaida? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khatib Said Haji, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, Serikali kwa nia thabiti kabisa imechukua hatua za kisera na benki zetu za kibiashara kwa kuanza wameanza na mikopo hii ya watumishi. Ni imani yetu kama Serikali benki zitashusha riba kwa wakopaji wote wakiwemo wakopaji wanaokopa kwa ajili ya biashara zao kwa kuzingatia watu hawa wanapatikana wapi na nini wanadhamiria kukifanya. Cha msingi nachotaka kuwaomba wafanyabiashara wetu ni kuwa na mipango thabiti wakati wanachukua mikopo hii ili kuhakikisha pesa wanazokopa zinaweza kurejeshwa na hivyo kuleta imani kwa benki zetu kwa wafanyabiashara wetu kwamba ni wakopaji wa uhakika na ni imani ya Serikali yetu kwamba riba zitaendelea kupungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba kwa kutambua umuhimu wa wajasiriamali wadogo, kwa kutambua umuhimu wa Watanzania wanaokwenda kukopa katika microfinances, Serikali yetu ya Awamu ya Tano ilizindua Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha Desemba, 2017. Dhamira kubwa ya sera hii ni kuhakikisha kwanza tunawatambua wakopeshaji kwenye huduma ndogo za kifedha lakini pia kuhakikisha tunawalinda wakopaji kwenye sekta hii ya huduma ddogo za fedha ili wawe na uhakika wanakopa nini na sheria, taratibu na kanuni za utawala bora ziweze kufuatwa hata kwenye sekta hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu inatambua mchango wa bei ya T-Bills. Sasa hivi tumeweza kupunguza bei ya T-Bills kwa kiwango kikubwa ili kuhakikisha pia bei ya fedha zinazokopeshwa inakuwa ndogo.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii na nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu vizuri na Serikali kuwa na mkakati mzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza deposit rate, maana watu wengi hawaweki fedha benki kwa sababu riba ni ndogo sana na riba ya kukopesha ni kubwa sana. Kama mkakati huu ukitekelezwa benki itakuwa na fedha nyingi ya kukopesha kwa riba ndogo. Naomba jibu, je, Serikali ina mkakati gani kuhusu suala hili?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la nyongeza la mtani wangu, Mheshimiwa Dkt. Mary Michael Nagu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali inashughulika na Sera ya Sekta ya Fedha na nimeainisha hatua mbalimbali tulizozichukua. Moja katika taratibu zilizopunguzwa ni statutory minimum reserve rates za mabenki yetu. Tumeona sasa, kama nilivyosema tangu awali, riba zinapungua na hivyo hata deposit rate nayo itaweza kuongezeka ili kuona kwamba Watanzania wanaweza kuweka fedha zao katika benki zetu.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza swali la msingi kumpongeza Rais kwa kupigania kupunguza riba kwenye benki, lakini kwenye taasisi ndogo ndogo, kwa mfano PRIDE, FINCA, Tunakopesha mpaka navyoongea sasa hivi riba inafika asilimia 33. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwadhibiti hawa watu wanaofikisha riba mpaka asilimia 33 na kusababisha akina mama kunyang’anywa vitu vyao kila siku? Maana yake pesa ile sasa inakuwa haizai kazi yake ni kurudisha riba inapofikia miezi sita mama yule anaanza kunyang’anywa vitu vya ndani. Mheshimiwa Waziri ana mkakati gani wa kukomesha tabia ya kufikisha riba asilimia 33?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la nyongeza la dada yangu, Mheshimiwa Munde, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, tumepitisha Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha na moja ya malengo yake ni kuhakikisha kunakuwa na uzingatiaji wa kanuni za utawala bora kwenye taasisi zinazotoa huduma kwenye sekta ndogo ya fedha. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Sheria ya Huduma Ndogo ya Fedha iko katika hatua za mwisho na ni imani yangu ndani ya mwaka huu sheria hii itapitishwa ili kuwalinda wakopaji wadogo katika sekta ndogo ya fedha. Naamini itakuwa ndiyo mkakati wetu na suluhisho la kuwalinda watu wetu.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nami naomba niulize swali moja tu. Kwa kuwa benki zote ziko chini ya Wizara ya Fedha na kwa kuwa CRDB wameanza kupunguza riba, je, kwa nini benki nyingine zisipunguze riba ili wananchi na wafanyabiashara waweze kupata mikopo kuliko hali ilivyo sasa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la nyongeza la kaka yangu Mheshimiwa George Lubeleje, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema kwenye jibu langu la msingi na nizipongeze Benki ya CRDB, NMB na ABC, benki zote hizi zimeshusha riba yao kutoka zaidi ya asilimia 20 mpaka asilimia 17. Ni imani ya Serikali kwamba benki zote zitafuata mwanzo huu mzuri ulioanzwa na benki hizi tatu nilizozitaja kama njia mojawapo ya kuakisi jitihada njema za Serikali ya Awamu ya Awamu ya Tano na Mheshimiwa Rais wetu dhamira yake ya kuhakikisha Watanzania wanapata fedha za mitaji kwa bei iliyo chini kabisa.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nadhani Mheshimiwa Naibu Waziri analifahamu vizuri suala hili la Kiwanda cha Nguo cha MUTEX, wale watumishi ajira yao ilikoma toka mwaka 1984 na baadhi yao mafao waliyopaswa kulipwa ilikuwa ni zaidi ya Sh.400,000 ambazo wao walizikaa kwamba hayo mafao yalikuwa ni madogo. Tumehangaika na suala hilo kwa kusaidiana na Mheshimiwa Waziri na hatimaye Desemba mafao yao yakatoka badala ya kulipwa zaidi ya Sh.400,000 wamelipwa chini ya Sh.100,000. Kwa sababu suala hili limechukua muda mrefu sasa, je, Mheshimiwa Naibu Waziri sasa yupo tayari kufuatana nami twende tukakae na hawa watumishi ili hilo suala liweze kuisha?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ameomba kuogozana nami kwenda Musoma Mjini, naomba nimwambie baada ya Bunge hili kuahirishwa ziara yangu ya kwanza ni kwenda Msoma Mjini kukutana na wastaafu hawa.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Swali langu linafafana na yaliyopita, kwa kuwa waliokuwa wafanyakazi wa TAZARA mwaka 2005 na mwaka 2009 wa miaka 55 walistaafishwa kwa lazima idadi yao ni 11,075. Ni lini wastaafu hao wa TAZARA watapewa mafao yao kwani mpaka sasa bado wanahangaika hapa Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Susan Kiwanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze nimeongea naye kuhusiana na jambo hili siku mbili zilizopita na baada ya kuongea naye nimelifuatilia jambo hili na naomba kuweka takwimu sahihi. Kwa takwimu tulizonazo ndani ya Ofisi ya
Msajili wa Hazina, wastaafu waliostaafishwa kwa lazima miaka 55 ni 271 na wala siyo 11,075 kama Mheshimiwa alivyosema. Hao ndiyo wastaafu tunaowajua ndani ya Wizara ya Fedha na Mipango na sasa hivi faili lao liko mezani kwangu Mheshimiwa Mbunge tangu nimeongea nawe tumeanza kufuatilia ili malipo yao yaweze kulipwa kwa wakati.
MHE. DEORATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Eneo la Manda ni bandari nzuri ambayo ingeweza kutumika ku-tap soko la nchi ya Malawi. Eneo la Malawi au nchi ya Malawi ina tatizo kubwa sana la bidhaa au vyakula kama mahindi na kadhalika ambako Ludewa mahindi yanalimwa kwa wingi kiasi ambacho mengine yanaoza kwenye maghala. Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kujenga hicho Kituo cha Forodha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namba mbili. Utaratibu wa kupata forodha ni kama ulivyoelezwa na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha. Je, baada ya kuandika proposal hiyo inachukua muda gani mpaka kukamilika kwake? Ahsante.
NAIBU WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Ngalawa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza alivyoanza kuipongeza Serikali kwa kufungua miundombinu kuwafikia wananchi ambao walikuwa hawajafikiwa nami naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naomba niwapongeze sana wananchi wa Manda kwa kazi kubwa wanayoendelea kuifanya ya shughuli za kiuchumi zinazowaondoa katika mzunguko wa umaskini kama ambavyo wenzetu wanaendelea kutangaza sifa za Taifa hili ambazo si sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwaambe Watanzania kwamba Taifa hili, alisema Mheshimiwa Waziri wa Fedha siku mbili zilizopita, kwamba kiwango cha umaskini kimepungua kwa kiwango kikubwa na sasa tunasubiri utafiti huu watakapotoa matokeo yao rasmi (household based survey) Watanzania wataona na wapuuze haya yote yanayoendelea kuenezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili nalisema kwa sababu sisi kama Serikali tunaitambua Manda kama eneo la kimkakati na ndiyo maana Bunge lililopita nilipojibu swali la 73 la Mheshimiwa Mbene kuhusu ujenzi wa Kituo cha Forodha Ileje na swali la nyongeza la Mheshimiwa Ngalawa nilimwambia tayari Serikali na namhakikishia tumeshaanza kufanya utafiti, tunachosubiri ni maombi hayo rasmi kutoka kwenye mkoa ili nasi tuifanyie kazi haraka iwezekanavyo.

Mheshimwa Naibu Spika, swali lake la pili, kwamba kwa muda gani unachukuliwa; kwa sababu tumeshaanza utafiti kama Serikali, namhakikishia, tutakapopata maombi hayo, tutayawasilisha rasmi Wizara ya Afrika Mashariki ili waweze kuwasilisha katika Sekretarieti ya Afrika Mashariki na haitachukua muda kwa sababu Manda ni eneo la kimkakati kwa Taifa hili.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia fursa hii. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, bado nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya Benki Kuu ya mwezi Februari, 2019 kwa maana ya Monthly Economic Review, inaonyesha kwamba kasi ya ukuaji ya ujazo wa fedha imeshuka kutoka asilimia 7.5 mwaka 2018 mpaka asilimia 3.3 mwaka 2019.

Je, Serikali haioni kuwa utekelezaji wa Sera ya Fedha umeleta matokeo tofauti kwa ukuaji wa ujazo wa fedha kuanguka zaidi kuliko mwaka 2018?

Swali la pili; kasi ya ukuaji ya mzunguko wa fedha nchini ni moja ya kiashiria muhimu sana cha kasi ya ukuaji wa uchumi; na ushahidi unaonyesha kwa miaka 20 kwamba unapokuwa na kasi ya ukuaji wa uchumi ya 7% maana yake kasi ya mzunguko wa fedha unakuwa katika double digit kati ya asilimia 12 mpaka 15. Kwa kutumia kiashiria cha mzunguko wa fedha na mfumuko wa bei, kwa nini Serikali isiache kutoa taarifa za uongo humu ndani ya Bunge na kwa Umma kwamba uchumi unakua kwa 7% ilhali hali halisi ni chini ya 4%.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nianze na swali lake la pili kwa sababu ameisingizia Serikali, ni kwamba Serikali siku zote inasema ukweli na haijawahi kudanganya Bunge, wala kudanganya sehemu yoyote. Nayasema haya kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Spika, katika Mkutano wa Nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara (SADC) uliomalizika wiki mbili zilizopita, Tanzania imepongezwa kwa ukuaji wa uchumi mzuri kwa mfululizo wa miaka mitano. Kwa hiyo, siyo kwamba Serikali inayasema haya ndani ya Bunge peke yake, hapana. Serikali inayasema haya ndani ya Bunge, nje ya Bunge na Shirika la Kimataifa la Fedha (IMF) kwa taarifa yake limeipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ukuaji mzuri wa uchumi kwa kuweka nyenzo nzuri zinazohakikisha ukuaji wa uchumi wetu kuwa imara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge tusiwadanganye Watanzania, uchumi wa Tanzania uko imara. Kwa Afrika Mashariki sisi ni wa kwanza na kwa Afrika sisi hilo ni jambo la kawaida. Nendeni kwenye google, m-google halafu mtajua nini tunachokisema. Uchumi wetu uko imara.

Mheshimiwa Spika, uchumi wetu uko imara na tuna uhakika kama ambavyo prediction zetu zilionyesha. Kwa mwaka 2018 tutakua kwa asilimia 7.2 kama prediction zetu zilivyoonyesha.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la kwanza, ni sahihi kabisa alichokisema kwamba ujazi wa fedha ukilinganisha mwaka 2018 na mwaka 2019 taarifa iliyotelewa na Benki Kuu, ujazi wa fedha umepungua. Hiyo haimaanishi kwamba uchumi haufanyi vizuri. Unaposoma ile taarifa, soma na sababu, kwa nini ujazi wa fedha umepungua?

Mheshimiwa Spika, ujazi wa fedha umepungua kwa sababu Watanzania sasa hata hapa ndani tukijaribu kuchukua simu ya kila mmoja wetu, ndani ya kila simu ya mmoja wetu kuna fedha za kutosha ndani ya simu yake na anafanya transaction electronically kwa siku zaidi ya jinsi ambavyo anafanya cash transaction kwa fedha taslimu halisi.

Kwa hiyo, kunapokuwa na ongezeko la transaction electronically, fedha halisi sokoni zinapungua, lakini fedha zilizopo kwenye mzunguko zipo za kutosha. Kama nilivyosema, sera yetu ya fedha inahakikisha mzunguko wetu wa fedha unalingana na shughuli za kiuchumi ambazo zinaendelea ndani ya Taifa letu.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba niulize maswali madogo tu mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, naomba niipongeze Serikali kwa majibu yake mazuri, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa tamko lake ambalo limehakikisha kwamba wazabuni wote wanalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna baadhi ya wazabuni wakiwemo hata wa Mkoa wangu wa Iringa wameshafanyiwa uhakiki zaidi ya mara moja, lakini wanadaiwa na mabenki, wanadaiwa na TRA na wanatishiwa mpaka kuuziwa mali zao:-

Je, Serikali inawasaidiaje wasifilisiwe? Maana wengi wao tayari wameshapata maradhi na kufa na wengine wameshafilisika kabisa kwa ajili ya madeni ambayo wanaidai Serikali.

Swali langu la pili; je, ni vigezo gani sasa vinatumika kwenye malipo ya madeni ya wazabuni hao?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la kwanza kuhusu msaada wa Serikali ili wananchi wetu wasifilisiwe, naomba kumwambia Mheshimiwa Rita na kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, tunalipa madai pale yanapokuwa yamehakikiwa. Wananchi wetu hawa wa Mkoa wa Iringa, kama wapo ambao madeni yao yamehakikiwa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Ndani wa Serikali, basi tumekuwa tukiwasaidia mmoja baada ya mwingine wanapofika na kuwasilisha nyaraka zao kuonyesha kwamba wamehakikiwa na sisi kujiridhisha kwamba wapo kwenye orodha ya kulipwa ndani ya Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Ritta na nimpongeze kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya katika kuwatetea wananchi wa Iringa. Ameshakuja siyo mara moja wala mara mbili ofisini kwangu, naomba tuendelee kushirikiana ili tuwasaidie wananchi wetu ili wasifilisiwe na ili wasiendelee kupata maradhi kama wapo kweli waliopata maradhi. Tuendelee kushirikiana tuwasaidie wananchi hawa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, ameuliza ni vigezo gani vinavyotumika kulipa madai haya ya wazabuni pamoja na wakandarasi wengine? Kwanza kabisa ni kuhakikisha deni limehakikiwa na limekidhi vigezo vya kuwa deni halali. Hicho ni kigezo cha kwanza kwamba deni hilo linalipwa.

Mheshimiwa Spika, sababu ya pili au kigezo cha pili ambacho kinapelekea kulipwa, tunaangalia deni lile kama hali-attract riba kwa Serikali, lakini pia kwa yule ambaye anaidai Serikali. Kama deni hili lina-attract riba tunayapa kipaumbele ili Serikali isiendelee kuumia na ili tusiendelee kuwaumiza wananchi wetu ambao wanaidai Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, kigezo cha tatu ni kuhakikisha kwamba ukubwa wa deni lenyewe, kwa wale ambao wana madeni ambayo siyo makubwa na ambao ndio wengi tumekuwa tukiwapa kipaumbele kuhakikisha kwamba tunawalipa madeni yao kwanza ili kuweza kuchachua uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana mwaka 2017/2018 Bunge lako Tukufu lilitupitishia bajeti ya shilingi trilioni moja kwa ajili ya kulipa madeni haya na Serikali ililipa zaidi ya shilingi trilioni 1.096 kwa sababu dhamira ya Serikali yetu ni njema kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Spika, kigezo cha nne, ni umri wa deni. Madeni yale ambayo yamekaa kwa muda mrefu na tayari yamehakikiwa, tumekuwa tukiyapa kipaumbele na kuhakikisha yote yanalipwa ili kuwawezesha wananchi wetu kuendelea kushiriki katika shughuli za kiuchumi.
MHE. MARY D. MURO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Swali la kwanza, ni kwa nini Serikali haikufikiri kabla haijaanzisha mradi huo wa maroli kupaki pale Misugusugu mpaka ikafikia wananchi wa Misugusugu wanapata TB?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nini mkakati wa Serikali wa dharura kwa ajili ya kuokoa maisha ya wana Misugusugu?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Deo Muro, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza kwa nini Serikali haikufikiri kabla, Serikali siku zote inafikiri, ilifikiri enzi hizo na sasa inaendelea kufikiri ili kuendelea kuboresha maisha ya wananchi wetu hasa hawa wa Misugusugu na ndio maana Wizara ya Ujenzi imeanza kuiboresha barabara ile ili kuondokana na changamoto hii ya vumbi pamoja na kwamba Serikali inatekeleza mradi huu wa Euro milioni 23 kuhakikisha sasa eneo lile la Misugusugu kituo kile kinaondoka na kinahamia vigwaza. Kuonesha kwamba Serikali inaendelea kufikiri na kutenda kwa ajili ya wananchi wake, haya tunayoyatenda Vigwaza yanakwenda kutendwa Manyoni na pia tunakwenda kutekeleza mradi wa aina hii kule Nyakanazi ili kuhakikisha huduma hizi zinafanyika kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, ni mkakati wa dharura, ndio huu ambao nimeeleza kwamba Serikali inaboresha barabara il, lakini tunahakikisha mradi huu unakamilika kwa wakati. Nitoe wito kwa Watanzania wote kwa ujumla maana ya kuwa na vituo hivi ni kuhakikisha mizigo ile yenye uhatarishi wa upotevu wa mapato tunaendelea kui-control hatua kwa hatua. Hata hivyo, pia wito wangu kwa Watanzania ni kuhakikisha kwamba wao wanakuwa wazalendo zaidi kwa Taifa lao ili mizigo hii ambayo wana- declare kwamba inaenda nchi jirani isiendelee kushushwa ndani ya Taifa letu. Unapoona gari linashusha mzigo ndani ya kijiji chako jiulize mara mbili kwa nini halikushusha mjini na lazima Watanzania wafahamu kwamba hakuna maendeleo bila kodi itakayolipwa na sisi Watanzania wenyewe na Serikali ya Awamu ya Tano imeonesha mfano na tunatenda kwa vitendo kwamba kodi ya Watanzania sasa inapelekwa kwenye miradi inayowafikia wananchi moja kwa moja.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri na ya kutosheleza kabisa, lakini nina swali moja dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Serikali imekuwa na zoezi la kuyafungia maduka ya Bureau De Change nchi nzima. Je, zoezi hili ni miongoni mwa mikakati ya kuimarisha fedha yetu au ni kwa madhumuni gani?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyouliza je, ulikuwa ni mkakati wa kuhakikisha thamani ya fedha yetu. Kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi moja ya kazi za benki kuu ni kuhakikisha kwamba thamani ya fedha yetu inakuwa imara na katika mikakati ya kuhakikisha hilo, ni kuhakikisha kunakuwa na usimamizi imara na madhubuti wa maduka yetu ya kubadilisha fedha na hilo ndilo lilikuwa lengo la zoezi lililofanyika.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Mheshimiwa Upendo Peneza bado ana maswali mawili ya nyongeza kutokana na majibu ya Serikali. Swali la kwanza, nauliza kwamba, japokuwa Serikali imeondoa baadhi ya kodi katika uzalishaji wa taulo za kike lakini bado bei ya taulo hizo iko juu sana. Sasa Serikali ina mkakati gani wa kusimamia bei hii kushuka ili kufikia wale walengwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, anauliza, sasa kama Serikali imeshindwa kusimamia kushuka kwa bei za hizi taulo japokuwa wameondoa baadhi ya kodi, je, haioni kwamba iendeleze tu kodi zile za awali lakini kodi hii ikusanywe na iwe ringfenced ili kuweza kununulia hizi taulo za kike na kuzigawa bure shuleni?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Sware Semesi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nianze na swali lake la pili ambapo amesema kama Serikali imeshindwa kusimamia kushuka kwa bei; naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Taifa letu kwa ujumla tupo katika soko huru kwa bidhaa zote, kwa hiyo sio kwamba Serikali imeshindwa kusimamia kushuka kwa bei, hapana, haijashindwa na ndiyo maana sasa hivi baada ya kuondoa kodi ile kwenye bidhaa hii Serikali imeendelea kupokea maoni mbalimbali ya wananchi wetu wakiwemo Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, ili kuweza kuweka bidhaa hii kuwa ringfenced Serikali inaendelea kufanya tafiti mbalimbali, lakini kuna changamoto ya kusema kwamba kodi inayotozwa specific kwenye bidhaa hii iwekwe kwa ajili ya wanafunzi hawa kwa sababu yapo makundi mengine ambayo kodi zinatozwa kwenye bidhaa zinazotumika specifically na makundi kadhaa, kwa hiyo tutatengeneza ombwe la kila kundi kuja kuomba kodi inayotozwa kwenye makundi hayo waweze kupewa wao.

Mheshimiwa Spika, Serikali kama nilivyosema inaendelea kufanya utafiti, tumekwenda nchini Afrika Kusini, Botswana na Kenya kujifunza nini wanafanya. Wenzetu waliondoa kodi hizi na wakagundua kwamba haiwezi kuleta matokeo chanya kama ambavyo yamekuwa ni majibu ya Serikali yetu ndani ya Bunge lako Tukufu. Kinachotakiwa kufanyika ni kubuni njia nyingine ya kuhakikisha watoto wetu wa kike wanapatiwa bidhaa hizi lakini bila kui-attach na kodi au tozo zozote zinazotozwa kwenye bidhaa hii kwa sababu tumejiridhisha kwamba unapoondoa kodi wanaonufaika ni wazalishaji kwa sababu tuko kwenye soko huria.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, kwamba ni mkakati gani kama Serikali tunaweka; nimesema sasa hivi tunaendelea kufanya tafiti mbalimbali ambapo tutakapojiridhisha na options ambazo zitaleta matokeo chanya kwa pande zote mbili watoto wetu wa kike na Serikali yetu, basi tutakuja na option hiyo ndani ya Bunge lako Tukufu ili tuweze kuwasaidia watoto wetu.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, ahsante, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri na ya kutoshereza kabisa, lakini nina swali moja la nyongeza.

Majibu yake yamejikita sana kwenye maeneo ya miji, swali langu ni kwamba Serikali ina mpango gani, huduma hizi kuzipeleka katika visiwa vidogovidogo kama vile Tumbatu?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema huduma zetu za TPB zimeongezeka kwa kiwango kikubwa na tumeweza kuwafikia wananchi walio wengi na kwa visiwa vyetu kwa Zanzibar tumeshafungua matawi tayari na sasa tunajipanga kwenda kufungua katika visiwa hivi vidogo, wakati huo tukiendelea kuwahudumia kwa kupitia mfumo wa kidigitali.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa tatizo hili sio mara ya kwanza kutokea hapa nchini, je, Serikali ina mkakati gani wa makusudi kuzuia jambo hili lisitokee tena kupunguza usumbufu kwa wananchi wetu?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, Serikali mikakati iliyonayo ni kusimamia sheria ya mabenki na taasisi za fedha ya mwaka 2006 kama inavyoelekeza kuhusu unazishwa na usimamiaji wa uanziswaji wa taasisi za kifedha ndani ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, na Serikali mmeona kwa sasa imekuwa, imeweka udhibiti wa hali ya juu kuhakikisha taasisi zote za kifedha zinafanya kazi kulingana na sheria ili kuzuia changamoto hizi wanazozipata wateja wetu.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kutokana na majibu ya Serikali, kuna mkanganyiko mkubwa na mlolongo mrefu kwa watu hawa kupata haki zao.

Sasa kwa kuwa Benki Kuu ndiyo guarantor wa hizi benki, kwa nini Serikali isimalizane na hawa wateja kwa niaba ya hii benki halafu Serikali sasa ibaki ikishughulika na benki hii wakati wananchi wakiwa wanaendelea na shughuli zao, hasa ikizingatiwa kuwa ziko taarifa kwamba, wamiliki wa benki hii wametushitaki, wameishitaki Serikali kutokana na hatua walizochukua?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, benki inapofilisika, benki inaponyang’anywa leseni yake ya kufanya kazi, hatua zote za ulipaji wa wateja wa beki hiyo au taasisi hiyo ya kifedha, imetajwa katika sheria ya mabeki na taasisi za fedha kifungu cha 39(2) na (3), ambako kuna maeneo mawili.

Mheshimiwa Spika, kwa wale ambao wana amana zilizo chini ya 1,500,000 hulipwa fedha zao zote, kwa wale ambao amana zao ni zaidi ya hiyo, hulipwa kwa kutumia sasa sheria ya ufilisi baada ya kujiridhisha na madeni na mali halisi ya benki hiyo au taasisi ya kifedha kama ilivyoelezwa.

Mheshimiwa Spika, lakini naomba niliambia Bunge lako Tukufu kwamba, siyo kwamba wamiliki wa benki ndiyo walioishitaki Serikali, hapana, waliostopisha mchakato huu ni Central Bank ya Cyprus, ambayo wao wanaona wana mandate ya kuweza kulipa wateja wote wa benki hii, wakisahau kwamba kulingana na sheria ya uanzishwaji wa mabenki, wanaotakiwa kulipa ni kule ambako benki hiyo ilikuwa na makao makuu, na makao makuu ya benki hii ya FBME yalikuwa Dar es Salaam lakini shughuli zake nyingi zilikuwa zinafanyika nchini Cyprus.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, mwezi wa nne tarehe 5 mwaka 2019, Serikali mbili zimekutana nchini Cyprus na tayari makubaliano yamefikiwa ya jinsi gani ya kuhakikisha wateja wote wa iliyokuwa benki ya FBME Tanzania na FBME Cyprus wanapata haki zao bila kupoteza chochote katika mchakato huu.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, wananchi wengi wameathirika kwa kukosa fedha zao ambazo waliziweka katika benki hii na Benki Kuu inapotoa leseni au kibali kwa ajili ya kufungua benki, wao wanakuwa ndiyo dhamana.

Mheshimiwa Spika, na kuna methali inasema dhamana ndiyo mlipaji, lakini hata mahakamani unapomchukulia mtu dhamana, akikimbia wewe ndiyo unakamatwa unahusika na suala lile. Kwa nini Benki Kuu isiwalipe hawa watu fedha zao, halafu wao wakaendelea na huo, kwa sababu watanzania wanaathirika na hili.

Sasa maana ya ninyi kuwa dhamana ni nini?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nimesema kwenye majibu yangu ya msingi, uendeshaji wa taasisi za kifedha yakiwemo mabenki imeelezwa wazi kwenye sheria ya mabenki na taasisi za kifedha ya mwaka 2006. Benki Kuu haiwezi kuwa dhamana na kuchukua jukumu la kulipa wateja wote ndiyo maana ikaanzishwa Bodi ya Amana, kama nilivyoeleza, ambayo ina dhamana kubwa ya kuwalipa wateja ambao wanamiliki amana chini ya 1,500,000.

Mheshimiwa Spika, na niseme kwamba, asema wateja wengi wamepoteza, kwa experience tuliyonayo ndani ya Taifa letu, iknapofungiwa benki yoyote au taasisi yoyote ya kifedha, zaidi ya asilimia 90 ya wateja wa benki au taasisi husika ya kifedha, huwa ni wale wenye amana ya 1,500,000 kurudi chini.

Kwa hiyo, hawa asilimia 10 iliyobaki, ndiyo nimesema kwamba, Serikali mbili zimeshakutana, mwezi Aprili, tarehe 5, 2019 na tayari tumeshakubaliana jinsi ya kuliendea jambo hili ili wateja wateja wote sasa waliobaki ambao ni zaidi, waliokuwa na amana ya zaidi ya 1,500,000, waweze kulipwa amana zao.
MHE. SALIM HASSAN ABDULLAH TURKY: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Ukiangalia juhudi za Serikali ya kukuza uchumi huu, sasa hivi jinsi hizi benki zinavyokwenda tunaanza kupata mshituko kidogo. FBME imezama, M Bank nayo imezama, M Bank kama ninafahamu ni benki ya Tanzania hatuwahitaji Ma-Cyprus kuja kutujibu, lakini bado zile dhamana ambazo ni za Serikali, naomba sana kwamba Serikali itoe tamko rasmi kwa sababu wateja ni wengi ambao wanahangaika na Serikali iko hapahapa na hii benki iko hapahapa, na sasa hivi imechukuliwa na benki nyingine ya Serikali yetu.

Kwa hiyo, tunaomba sana tujulishwe hii hatma ya kudai fedha za M Bank, tunazipata vipi kwa uharaka wake? Ili watu waamini kuweka fedha benki maana sasa hivi sasa watu kuweka fedha benki tunaanza kuogopa, tunaona hizooo, zinazama.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kuna usalama mkubwa sana ndani ya Taifa letu, kwenye taasisi zetu za kifedha kwa sababu Benki Kuuu ya Tanzania iko macho na iko makini kusimamia sheria ya kuazisha benki hizi na taasisi za kifedha.

Mheshimiwa Spika, na niliombe sana Bunge lako Tukufu, tunapokuja na sheria ya kusimamaia hizi taasisi za kifedha, muwe mnatuunga mkono, ni kwa sababu tunaona wengi wa wateja wetu wanapoteza fedha kwa kuingia katika mifumo ambayo siyo sahihi na nilishukuru Bunge lako Tukufu kwa kuturuhusu kwenye Bunge letu la mwezi wa 11 kupitisha sheria ya huduma ndogo za fedha na sasa tunawafikia wote kule walipo ili kuhakikisha wateja wetu wote wanakuwa salama.

Mheshimiwa Spika, na niseme, hili la M Bank, kama alivyosema muuliza swali, M Bank imechukuliwa na benki nyingine. Kwa maana hiyo, M Bank siyo kwanza wataja wake wanatakiwa kusubiri mchakato kwa sheria ya ufilisi, hapana. Benki iliyoichukua M Bank, ina jukumu na dhamana kubwa ya kuhakikisha wateja wote wanalipwa na wanalipwa amana zao zote pale wanapozihitaji.

Mheshimiwa Spika, lakini niwaambie watanzania kwamba, kuweka fedha zao kwenye benki zetu ni salama na benki ambayo M Bank imeunganishwa inafanya vizuri na niwaombe waendelee kuacha amana zao huko kwa sababu faida ni kubwa ya kuacha fedha zao kwenyeakaunti zao.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Wilaya ya Ngara ni sehemu ya Mkoa wa Kagera na ni Wilaya inayopakana na nchi mbili kwenye Mpaka wa Rusumo kwa maana kupakana na nchi ya Rwanda na mpaka wa Kabanga kupakana na nchi ya Burundi. Kama alivyojibu Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha, kwenye mipaka hii kuna vituo vya pamoja vya forodha, lakini ipo fursa ya masoko ambayo hatunayo sasa na hivyo kupelekea wananchi wetu washindwe kufanya biashara katika maeneo haya ya mipakani.

Je, Serikali ipo tayari kutenga fedha kwa ajili ya kujenga masoko maeneo hayo ikiwezekana shopping malls ili kunufaika na fursa hii?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Halima Bulembo na swali lingine la Mheshimiwa Gashaza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na swali la Mheshimiwa Halima Bulembo kuhusu kujenga kituo kikubwa cha biashara cha Afrika Mashariki katika Mkoa wa Kagera, napenda kulitaarifu Bunge lako tukufu kwamba Serikali yetu ipo katika mpango mkakati wa kujenga kituo kikubwa cha kibiashara pale katika eneo la Nyakanazi ambapo soko hili litaweza kufikiwa na wananchi wetu wa mikoa inayozunguka Kagera, lakini pia nchi za DRC, Burundi, Rwanda na Uganda wote watakuwa na fursa ya kufika pale Nyakanazi kwenye kituo kikubwa hiki ambacho Serikali yetu kwa kushirikiana na Halmashauri zetu imeanga kukijenga kuanzia sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye swali la Mheshimiwa Gashaza kuhusu Serikali kutenga fedha kwa ajili ya kujenga masoko haya pale Rusumo na Kabanga, nilifika pale Kabanga na kuona hali halisi ilivyo na tayari upo mradi ambao unaendelea wa ujenzi wa soko la kimataifa pale Kabanga ambapo naamini ndani ya miaka miwili litakuwa limekamilika na wananchi wetu watakuwa wamefikiwa ili waweze kuuza mazao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo, kule Rusumo pia Serikali ipo kwenye mpango wa kuhakikisha tunaanzisha soko ili kuhakikisha sasa wananchi wetu wa Kagera wananufaika na jiografia yao ya kupakana na nchi zilizozunguka.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza:

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niipongeze sana benki ya TPB kwa kufanya kazi vizuri na kuendele kujiboresha, nina maswali mawili ya nyongeza ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, moja ya sababu ya kuanzisha benki zinazosimamiwa na Serikali popote duniani, sababu za kuanzisha Benki za Umma ni kwenda kua-address mapungufu ambayo sekta binafsi, Mabenki Binafsi yameshindwa kuyashughulikia. Miongoni mwa mapungufu hayo ambayo tunayo hapa Tanzania ni kwamba Wajasiriamali wengi wadogo wanashindwa kufanya biashara zao kwa sababu hawana mitaji, ni kwa namna gani Benki hii ya Posta inajitofautisha na benki zingine za kibiashara katika kusaidia Wajasiriamali wadogo nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu ya pili swali langu tumeona kwamba Benki ya Kilimo Tanzania haina matawi katika Mikoa mingi na Wilaya nyingi na Wakulima wanakosa mitaji ya biashara ni kwa namna gani sasa Serikali imejipanga kuitumia Benki ya Posta kama Tawi kama tawi la Benki ya Kilimo Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ni jinsi gani TPB inajitofautisha katika kutoa huduma na benki nyingine za biashara, naomba kumpa taarifa kwamba Benki ya TPB kwanza ina Matawi katika Mikoa yote Tanzania na imekwenda katika Wilaya ambazo tunasema ni kama Wilaya za Vijijini ambako Mabenki mengi ya biashara hayajafika, kwa hiyo hilo ni jambo la kwanza walilolifanya kuwafikia wananchi wetu kule walipo. Pia, Benki ya TPB ina mfumo wa kukaa na Wajasiriamali kuwapa mafunzo na kuwapa mikopo ambayo ina riba nafuu ikishirikiana na Benki yetu ya Kilimo Tanzania.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, ni jinsi gani inaweza kushirikiana naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Bunge lako Tukufu tayari Benki yetu ya Kilimo ilishafungua matawi yake kwenye Kanda, Kanda ya Mwanza na Kanda ya Kati, tayari wameanza kufanya kazi na sasa wanajiandaa kwenda kufungua Tawi lao Mkoani Mbeya ili kuhudumia Nyanda za Juu Kusini. Wakati tukiendelea kufungua matawi ya Benki yetu ya Kilimo, Benki ya Kilimo pamoja na Benki ya TPB wanashirikiana na kwa mwaka huu wa fedha peke yake wametoa mikopo zaidi ya bilioni 431 kwa wakulima wetu kwenye maeneo yale ambapo TADB haina matawi lakini TPB imeweza kufika.

Mheshimiwa Spika, ni imani yetu sisi kama Wizara tunayosimamia sekta hii kuhakikisha kuwa wananchi wetu wakiwemo wajasiriamali wadogo pamoja na Wakulima wetu wanafikiwa na huduma hizi kupitia Benki hizi za Umma zinazoendeshwa kwa kodi zao.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Rufiji ni Wilaya kongwe sana iliyozaa zaidi ya Wilaya tano lakini pia imezaa Taifa la Fiji kama ambavyo wewe mwenyewe unafahamu. Lakini pia eneo la Rufiji, Kibiti na Kilwa hakuna benki yoyote ya biashara na Serikali sasa inapeleka zaidi ya trilioni saba za ujenzi wa uzalishaji wa umeme katika Bwala la Mto Rufiji ambapo tunategemea kuwepo kwa watumishi, wafanyakazi zaidi ya 6,000 mpaka 7,000.

Je, Serikali haioni umuhimu sasa kwamba tawi la benki katika Wilaya yetu ya Rufiji haliepukiki? Hilo swali la kwanza.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, eneo la Rufiji lina ukubwa wa zaidi ya hekari 500,000 ambao lipo ndani ya Bonde la Mto Rufiji, lakini pia kwa kuwa Serikali inatekeleza Mradi wa Umeme wa Rufiji, Serikali pamoja na Wilaya ya Rufiji imetenga zaidi ya hekari 150,000 kwa ajili ya kwenye kilimo cha kisasa cha umwagiliaji.

Je, Serikali haioni umuhimu sasa kwamba Benki ya Maendeleo ya Kilimo ni muhimu sasa kuwepo Rufiji ili kuweza kuwasaidia wananchi wa Rufiji kuchangamkia fursa za maendeleo, fursa za kilimo, fursa za biashara katika Mradi wetu wa Umeme wa Rufiji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa, Mbunge wa Rufiji, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza kuhusu kwamba Serikali haioni kwamba haiepukiki sasa kufungua tawi Rufiji, kama nilivyosema benki nyingi zinaendeshwa kibiashara na benki nyingi huwa zinaangalia commercial viability ya eneo husika kabla hawajaweza kupeleka tawi la benki husika kwenye eneo husika. Kwa hiyo, kama ambavyo nimesema kwenye jibu la msingi, mabenki yetu yanafanya utafiti huo na tathmini kujiridhisha na nini kinatakiwa kufanyika kwenye maeneo husika. Hata hivyo, nimwambie Mheshimiwa Mchengerwa kwamba baada ya swali lake hili kama Serikali tumeanza kuifanyia kazi na tumeongea na Mkurugenzi wa TPB PLC na Mkurugenzi ameomba yafanyike yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza anaomba apate maombi mahsusi ili kuweza sasa kutuma timu yake kwenda kufanya kufanya feasibility study na kujiridhisha na commercial viability ya eneo la Rufiji ili kwenda kufungua tawi la Benki ya TPB kutokana na potentials zote kama zilivyoelezwa na Mheshimiwa Mchengerwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili kuhusu Benki ya Kilimo, kama alivyosema yeye mwenyewe Benki ya Kilimo ni benki ya maendeleo, hivyo lazima kila inapokwenda kufunguliwa ielewe kabisa wanakwenda kuhudumia aina gani ya wananchi ambao wako kwenye miradi mikubwa ya kimaendeleo. Pia Rufiji hawako mbali sana na Dar es Salaam ambako Benki yetu ya Kilimo ya Maendeleo ndipo Makao Makuu yake yalipo ambapo inahudumia maeneo yote ya Pwani, maeneo ya Morogoro. Kwa hiyo, niwaombe sana wakulima wetu wakubwa ambao wanahitaji mikopo ya maendeleo wafike Dar es Salaam na watahudumia na Benki yetu ya Kilimo ya Maendeleo. (Makofi)
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Wilaya ya Igunga kwa kupindi cha miaka mitano sasa shughuli zake za uchumi zimeongezeka sana, watu wanalima, watu wanafuga na kuna fedha nyingi mzunguko ni mkubwa, lakini tatizo ni kwamba tuna benki moja tu Benki ya NMB. Benki ya CRDB walikuja wakafanya evaluation wakaona economic viability pale ni nzuri na wakaja wakatembea, lakini mpaka sasa hivi hawajaanzisha benki. Naomba Serikali, ni wakati sasa kama wanaweza kutusaidia kuiambia Benki ya CRDB wafungue tawi pale Igunga. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Peter Dalaly Kafumu, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimepokea taarifa yake ya kwamba Benki ya CRDB ilifika na kufanya economic analysis na commercial viability ya Wilaya yetu ya Igunga, na mimi nimepokea maombi yake, nitawasiliana na Mkurugenzi Mkuu wa CRDB kuhusu kujua utafiti huo umefika wapi na nini maamuzi yao, kama inaonekana kuna commercial viability nina uhakika mkubwa kwa sababu CRDB ni moja ya benki inayowafikia wananchi, watafika Igunga.
MHE. RHODA E. KUMCHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na changamoto za kukosa huduma za kibenki katika Mkoa wa Katavi, Wilaya ya Mlele pamoja na Wilaya ya Tanganyika ni moja ya Wilaya ambazo zinakosa huduma za kibenki na ukizingatia asilimia 80 ya wakulima walioko kule wanafanya biashara kubwa na wana pesa nyingi wanasafirisha kwa njia ya magari. Sasa usalama wa fedha zao kutoka katika Wilaya hizi wanatembea zaidi ya kilometa 60 mpaka katika Wilaya ya Mpanda.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha tunapata matawi ya kibenki ili wakulima hawa waweze kusafirisha fedha zao katika mazingira yaliyo salama? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Rhoda Kunchela, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, inashangaza kidogo kusema wananchi bado wanasafirisha pesa kwa magari wakati Serikali imefungua na imeongeza mawanda mapana kabisa ya huduma za kibenki hapa nchini. Hakuna eneo lolote utakapofika hapa nchini ukakosa huduma za kifedha za mawakala wa benki zetu mbalimbali na huduma za simu banking katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, ndio maana Tanzania inaongoza kwa Afrika kwa huduma za fedha jumuishi. Kwa hiyo, niwaombe sana wananchi wetu Wilaya ya Mlele, Wilaya ya Katavi waweze kuzitumia fursa hizi zilizopo baada ya Serikali yao kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara nchini. Mawakala wengi wa huduma za fedha wapo kwenye maeneo yote nchini na sasa kila mwananchi ana simu yake, tumeweza kusajili simu kwa hiyo sasa hivi ni rahisi sana kufanya transactions.

Sasa hivi unapofanya transaction niwaambie wananchi wa Tanzania huna wasiwasi wa kutuma pesa yako kwa simu kwa sababu mfumo umeunganishwa na Benki Kuu ya Tanzania, kwa hiyo, unajua kabisa kabla hujatuma kuliko kukaa na kuanza kufikiri fedha yangu imepotelea njiani, sasa unaulizwa kabisa unamtumia fulani bin fulani, una uhakika kwa hiyo hakuna wasiwasi wowote. Niwaombe Watanzania watumie fursa hii ya huduma za fedha jumuishi kwa maendeleo yao na maendeleo ya Taifa letu.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali ambayo yametolewa na Naibu Waziri, lakini mimi shida yangu ni moja tu. Mimi sio Mhasibu sana lakini ukitazama ukweli uliopo ni kwamba ukaguzi huu ambao ni wa Kimataifa unaonyesha nyaraka za kihesabu na vitabu vya kihesabu vinavyokaguliwa kama viko sawa, lakini havionyeshi matumizi ya ndani kama shirika limepata hati safi kwa maana kwamba halina ubadhirifu. Sasa je, Serikali inaonaje sasa, utaratibu wa Kimataifa uendelee lakini tuwe na utaratibu wa ndani ili kutambua ubadhirifu unaotokea kwenye mashirika yaliyo na hati safi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba kuna dhana ya ukaguzi ambapo wanaona kama kuna matatizo makubwa yanatokea kwenye athari za kihesabu; sasa haya matatizo makubwa na haya madogo anayoyataja sijayaona kwenye majibu yake; pengine angeweza kutusaidia kwamba haya matatizo makubwa ya kiathari za hesabu ni yapi kwenye shughuli za kimahesabu?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nayajibu maswali yake yote mawili kwa sababu yote jibu lake ni moja. Zipo aina tofauti za kaguzi zinazofanyika ukiacha kaguzi za mahesabu kama nilivyosema ili kujibu maswali yake yote mawili kwamba ni matatizo gani makubwa na madogo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kunapokuwa na matatizo hayo mengine ambayo yako nje ya taarifa za kihasibu, huwa kuna ukaguzi wa ufanisi (performance audit) ili kuweza kuijuza Serikali juu ya namna bora ya kutumia rasilimali zake katika kubana matumizi; pia kuhimiza taasisi za Umma kuboresha utendaji wake wa kazi kufikia malengo kwa tija na kupata thamani halisi ya fedha.

Kwa hiyo, hapa tunakwenda kwenye miradi yenyewe kuangalia mchakato mzima wa mradi ulifanyikaje na mradi je, unajibu hali halisi ya thamani ya fedha kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna aina ya pili ya ukaguzi ambayo ni ukaguzi maalum (special audit). Ukaguzi huu maalum huombwa maalum na mtu specific au taasisi yenyewe ikiwa imegundua kuna matatizo hata kama taasisi yake ina hati inayoridhisha. Kwa hiyo, hii inakuwa na hadidu za rejea ambazo zimetolewa na mtu aliyeona kuna matatizo kwenye taasisi hiyo kwa hiyo inafanyika special audit ili kujibu hayo matatizo yaliyoonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna ukaguzi wa kiuchunguzi (forensic audit). Huu ni ukaguzi wa kisayansi ambao nao unakuwa na hadidu za rejea, tunakwenda zaidi ya special audit kujua matatizo haya yamesababishwa na nini kwenye taasisi husika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tuendelee kuziamini ofisi zetu na hasa Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa sababu wanafanya kazi zao kitaalamu zaidi.
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya dada yangu Mheshimiwa Dkt. Ashatu, nina maswali mawili tu madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; malipo ya wachezaji na makocha wengi wa kigeni hapa Tanzania yanafanywa kiholela, hakuna mfumo rasmi:-

(a) Je, Serikali inatambuaje kwamba fulani kalipa na fulani hajalipa?

(b) Nchi zilizoendelea kama Uingereza, kodi ni jambo muhimu sana kwa wachezaji wa mpira wa miguu na hakuna kukwepa. Je, Serikali hapa Tanzania ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba vilabu vya ligi daraja la Premier na ligi daraja la kwanza wanapopata ajira kwenye vilabu hivi wanalipa kodi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza kujua nani kalipa na nani hajalipa kama nilivyosema, kulingana na Sheria ya Kodi ya Mapato ya Mwaka 2004, kila mtu anayepata mapato ndani ya Taifa letu anastahili kulipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jukumu la mwajiri kwenda kut oa taarifa Mamlaka ya Mapato Tanzania ya waajiriwa wake alionao wanaotakiwa kulipa kodi hiyo. Kwa hiyo, niwatake tu timu zetu zote ambazo zinaajiri makocha na wachezaji kutoka nje ya nchi ; kwenye mikataba yao, maana msingi wa kulipa kodi ya mapato na kodi ya ajira, kwanza kodi ya mapato ni lazima mlipaji yule awe ni mkazi ndani ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyofahamu, pia kwa kodi hii ya mapato, kila mgeni akifikisha zaidi ya miezi sita anahesabika ni local resident na anatakiwa alipe kodi hiyo na mwajiri wake, anatakiwa kutoa taarifa hiyo ili kodi hiyo iweze kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyeki ti, kwa hiyo, ni mhaki kishie tu kaka yangu kwamba waajiriwa wote wanatakiwa kulipa kodi hii kulingana na Sheria za Taifa letu zinavyoelekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuh usu swali lake la pili kwamba wanalipa kiholela n a wengin e yawezekana wan alipwa fedha hizi mkononi ; kama nilivyosema, ni jukumu la mwajiri kutoa taarifa ya nani analipwa nini ndani ya klabu yake ndani ya taasisi yake na ndani ya kampuni yake ili kodi zote zinazostahili kulipwa na hasa kodi ya mapato ambayo ni ngumu kulipika iweze kulipwa kama sheria zetu zinavyotakiwa kutekelezwa kwa vitendo.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kuunganisha Benki hii ya Wanawake pamoja na Benki ya Posta Tanzania. Kwa nini naipongeza? Naipongeza kwa sababu Benki ya Wanawake Tanzania ilikuwa katika maeneo machache hususani Dar es Salaam na maeneo mengine, haikuwa katika mikoa yote, lakini Benki ya Posta iko kila eneo la Tanzania hii, naipongeza sana Serikali yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu lipo hapa, katika hiyo Benki ya Posta ya Tanzania kuna akaunti moja inaitwa Tabasamu kwa ajili ya wanawake. Nadhani watu wengi hawaielewi, leo Mheshimiwa Naibu Waziri atueleweshe hapa. Je, hii akaunti ya Tabasamu imewasaidia kwa kiwango gani wanawake wa Tanzania katika kuwainua kiuchumi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la moja la nyongeza la Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Dada yangu Mheshimiwa Faida kwa kuwa yuko mstari wa mbele kufuatilia maslahi mapana ya wanawake wa Tanzania. Niwapongeze sana wanawake wa Zanzibar kwa kutuletea kifaa hiki na kinafanya kazi sawasawa kwa ajili yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili kwa sababu hata swali lake aliloliuliza, kauliza specific ili wanawake waendelee kufahamishwa nini faida wanayopata baada ya Benki ya Wanawake Tanzania kuunganishwa na Benki ya TPB.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefungua akaunti ya Tabasamu ni sahihi kabisa, Dada yangu Mheshimiwa Faida na akaunti hii maalum imefunguliwa kwa ajili ya wanawake wa Tanzania pekee, waweze kuhudumiwa kama wanawake kama walivyokuwa wakihudumiwa na Benki yao ya Wanawake Tanzania. Kwa hiyo, huduma zote zile zinatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nyongeza katika akaunti hii ya Tabasamu kama lilivyo jina lake, tunataka kupeleka Tabasamu kwa mwanamke wa Tanzania. Tunahitaji mwanamke wa Tanzania awezeshwe kupata mkopo wenye riba nafuu, awezeshwe yeye peke yake siyo lazima awe kwenye kikundi kama ambavyo mabenki mengine yanafanya, aweke akiba yake kidogo kidogo apate mkopo nafuu na aweze kufanya shughuli zake za ujasiriamali, afanye shughuli zake za kiuchumi na za kijamii kwa ajili ya maslahi yake yeye mwenyewe binafsi na maslahi mapana ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe wito kwa wanawake wa Tanzania, tuitumie akaunti hii ya Tabasamu ndani ya Benki yetu ya Posta. Imeanza vizuri na sisi tuko tayari kuwahudumia wanawake wa Tanzania kwa sababu Serikali ya Chama cha Mapinduzi inawajali Watanzania na hasa wanawake. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, mbali na Kituo cha Kabanga, kuna Kituo kidogo cha Forodha cha Murusagamba ambacho kinalelewa na Kituo cha Kabanga. Je, Serikali ina mkakati gani wa kupandisha hadhi Kituo hiki cha Murusagamba ili kiweze kuwa kituo kamili hasa kwamba upo mkakati wa kuunganisha barabara ya lami kutoka Nyakahura – Murusagamba - Burundi route ambayo pia itaendelea kuwa karibu? (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa sasa hivi ina Vituo vya Forodha vipatavyo 97 na upandishwaji wa Vituo vya Forodha kutoka kuwa vituo vidogo kuwa vituo kamili vya forodha huwa vina criteria yake ambayo na Kituo cha Murusabanga nacho tutaendelea kukifanyia kazi na tathmini. Kikikidhi vigezo vya kupandishwa hadhi na kuwa kituo kamili cha forodha kutokana na shuguli nyingi za kiuchumi zinazofanyika maeneo yale, Serikali haina shaka kukipandisha kituo hicho na Mheshimiwa Mbunge wa Ngara tuko tayari kufika tuweze kufanya tathmini hiyo.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Urejeshwaji wa kodi kwa wakati kwa makampuni ambayo yamewekeza nchini kutasaidia kuimarisha uwekezaji nchini na hivyo kuimarisha kipato cha mtu mmoja mmoja; je, Serikali ina kauli gani juu ya hili?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali moja la nyongeza la mdogo wangu, Mheshimiwa Khadija Nassir, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ameuliza kuhusu urejeshwaji wa kodi, naamini ni Kodi ya Ongezeko la Thamani, kwa wanunuzi na viwanda vyetu. Kama Taifa tunatambua kwamba tulikuwa na changamoto kubwa ya udanganyifu kwenye eneo hili la urejeshwaji wa Kodi ya Ongezeko la Thamani. Hivyo kama Serikali tulianza mkakati wa kuhakikisha tunajiridhisha na kila muamala ambao unaletwa ili kuweza kurejesha Kodi hii ya Ongezeko la Thamani kwa wazalishaji wetu, wanunuzi wetu pamoja na viwanda vyetu ambavyo viko hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi tayari tumeshalipa zaidi ya asilimia 90 ya Kodi hii ya Ongezeko la Thamani kwa watu ambao walikuwa wanatudai. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hii asilimia 10 iliyobaki Serikali tunaendelea kujiridhisha na uhakika wa miamala yenyewe na tutazirejesha kwa wakati.
MHE. MATTAR ALI SALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, ameeleza suala la sheria tofauti. Nimfahamishe Kenya na Tanzania tuna sheria tofauti, Uganda na Tanzania kuna sheria tofauti lakini bado magari ya Kenya yanapewa kibali kwa urahisi kuweza kutembea Tanzania Bara lakini magari yanayotoka Zanzibar mpaka uweke deposit (pesa nyingi) ambapo ndiyo unaweza kupewa kibali cha kutembelea Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimuulize Mheshimiwa Waziri wana utaratibu gani utakaokuwa rahisi kuweza kusaidia watu wa Zanzibar kuweza kutembelea gari ndani ya Tanzania Bara? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la Mheshimiwa Mattar, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu rahisi uliopo ni huo uliopo sasa mpaka pale sheria nilizozieleza kwenye jibu langu la msingi zitakaporekebishwa kwa pamoja.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, wazabuni wengi na nina imani hii ni kwa nchi nzima lakini hapa niwe specific kwa Tabora, ni wafanyabiashara wadogowadogo na wengi wapo sokoni wamekuwa waki-supply vyakula mbalimbali Serikalini kwa maana ya magereza na hata shuleni. Wengi wa wazabuni hao pamoja na kuhakikiwa madeni yao, hawajalipwa kuanzia mwaka 2013, inafika miaka sita (6) sasa na wazabuni hawa wengi wamekopa kwenye mabenki. Leo hii wengine wameuziwa nyumba zao na wengine wana kesi mbalimbali mahakamani. Serikali inasemaje kuhusu suala hili la kuwalipa wazabuni hawa kwa sababu madeni yao ni ya muda mrefu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kumekuwa na mtindo wa walipaji ambao wapo kwenye malipo mbalimbali hayo ya wazabuni kulipa madeni ya karibuni yaani wao kwa mfano deni ni la mwaka huu au la mwaka jana wanalipa hayo kwanza, yale ya miaka mingi ambayo watu wamekuwa na madeni haya ambayo yamepelekea mpaka kuuza nyumba zao hawalipi. Serikali inasemaje kuhusu hilo suala hilo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mwakasaka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza kwamba wapo wazabuni tangu 2013 hawajalipwa. Naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu kama nilivyosema kwenye jibu la msingi imekuwa ikilipa madeni haya kila mwaka. Kuanzia mwaka 2016/2017 tulitenga bajeti ya shilingi bilioni 625 na tukalipa shilingi bilioni 746. Mwaka 2017/2018 tulitenga shilingi trilioni 1 kwa ajili ya ulipaji wa madeni na tukalipa shilingi trilioni 1.096. Mwaka 2018/2019 tumetenga shilingi bilioni 600 na tukalipa shilingi bilioni 600.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeendelea kulipa madeni haya. Sasa linalonishangaza ni kusema kuna wazabuni wadogowadogo wa tangu mwaka 2013. Naomba nitoe wito wangu kwa Makatibu Tawala wa Mikoa wote waweze kuwasiliana na wazabuni kwenye mikoa yao ili wahakikishe kama madeni yao bado ni halali kwa sababu madeni yote ambayo ni halali tumekuwa tukiyalipa mpaka mwaka 2020/2021 tutakuwa tumekamilisha kulipa madeni yote na deni lililopo sasa ni shilingi bilioni 325 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili ni kwa nini wanalipa madeni ya karibuni. Tuna vigezo vya ulipaji wa madeni haya, kigezo kimojawapo ni kuhakikisha kuwa madeni ya zamani yanapewa kipaumbele kwenye kulipwa. Kwa hiyo, nitoe wito wangu kwa Maafisa Masuuli wote wanapopelekewa fedha za kulipa madeni wafuate vigezo walivyopewa na Mlipaji Mkuu wa Serikali ili tuweze kuwasaidia wazabuni wetu.
MHE. JOYCE B. SOKOMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante, niseme tu, sawa majibu ni marefu lakini hayajaniridhisha. Kwa mujibu wa sheria Mfilisi anapofilisi kiwanda au anaponunua kiwanda ni lazima kuwalipa wafanyakazi wote malimbikizo ya madai yao yote. Je, ni sahihi madeni ya msingi ya wale wananchi yapotee bure?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; hivi Serikali ilichukua hatua gani ili kwa aliyenunua kile kiwanda kuhakikisha wanawalipa wafanyakazi wale stahili zao zote toka shilingi 400,000, hatimaye wakawalipa laki moja, zile laki tatu zitalipwa lini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kulieleza Bunge lako Tukufu kwamba Serikali haiko tayari kuona Mtanzania yeyote wa aina yeyote akipoteza stahiki zake mahali popote ndiyo maana kwenye jibu langu la msingi nimeeleza kwa urefu jitihada zote ambazo Serikali imechukua kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu za ufilisi. Kwa hiyo, hakuna Mtanzania yeyote au mtumishi yeyote wa kiwanda hiki ambaye stahiki zake zitapotea.

Mheshimiwa Spika, nimeeleza wazi; watumishi 512 walilipwa tangu mwaka 1994 kulingana na sheria, kanuni na taratibu zinavyoelekeza, hawa waliokataa wamekwenda mahakamani zaidi ya mara mbili na wote mahakamani walikokwenda malalamiko yao yametupiliwa mbali, wameelekezwa kurudi kwa mfilisi. Ni mfilisi ndio anayetoa fedha hizi za kulipa baada ya kuwa ameshalipa madeni mbalimbali ambayo kiwanda hiki kilikuwa kinadaiwa, kinachobaki ndicho wanacholipwa watumishi hawa.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameuliza aliyenunua kiwanda hiki anatakiwa kulipa. Kulinaganga na sheria na kanuni na taratibu za ufilisi anayetakiwa kulipa siyo aliyenunua kiwanda, aliyetakiwa kulipa ni Serikali kwa sababu Serikali ndiyo iliyokuwa inamiliki kiwanda hiki na ndiyo maana mpaka leo Ofisi ya Msajili wa Hazina inashughulikia watumishi 312 waliobaki ili wakiwa tayari waweze kulipwa shilingi milioni 20 kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi. Kwa hiyo aliyenunua kiwanda hiki hana liability yoyote ya kuwalipa watumishi hawa na Serikali tuko tayari kuwalipa kwa wakati wowote.
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru, lakini ningemuomba Mheshimiwa Waziri kama atakubali ombi langu la kuongozana na mimi ili akaangalie jinsi gani wananchi wanavyokadiriwa makadirio ya juu yasiyokuwa na haki na kuwapa usumbufu mkubwa hasa wale ambao wanaishi katika maeneo ambayo hayajapimwa.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; je, ni lini Serikali itaifanya sasa Wilaya ya Mbagala kuwa mkoa wa kikodi ili waweze kukusanya vizuri kodi katika maeneo yasiyopimwa, yameachwa kwa asilimia nyingi sana na wanashindwa
kufikia huko kwa sababu TRA hawana man power ya kutosha? Kama hawawezi basi warudishe kwenye halmashauri zetu ili waendelee na zoezi hili.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la kwanza, wananchi kukadiriwa gharama kubwa kwa ajili ya kulipa kodi ya majengo. Naomba niwaambie wananchi wa Tanzania kwamba dhamira njema ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli ya kuhakikisha Watanzania hawaumizwi tena na kodi hizi tayari Bunge hili lilishapitisha sheria.

Mheshimiwa Spika, sasa kila jengo ambalo ni la chini ni shilingi 10,000 kwa hiyo hakuna anayelipa zaidi ya 10,000 kwa kila jengo ambalo ni la chini na kwa majengo ya ghorofa kwa kila ghorofa moja naomba niwaambie Watanzania kwa kila floor ya ghorofa lako ni shilingi 50,000 kwa hiyo hakuna makadirio yoyote ambayo yako juu na Mheshimiwa kaka yangu Issa Ali Mangungu niko tayari kwenda na wewe Mbagala tukaongee na wananchi wetu tuwaeleweshe nini dhamira ya Serikali yao na nini tumeanza kutekeleza.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili; hili ni jambo la kiutaratibu, naomba nilichukue tutakwenda kulifanyia kazi ili tuone ni lini sasa Wilaya ya Mbagala inaweza kuwa sasa ni Mkoa wa Kikodi ili tuweze kushughulikia ukusanyaji wa kodi hii kwa ufanisi.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa unyenyekevu mkubwa ninakupongeza wewe, na nichukue nafasi hii kukupongeza kwa kuwa mfano bora kutokana na miundombinu ya taasisi unayoingoza, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa rafiki, kila sehemu unapokwenda kwa kweli imejali mahitaji ya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa moyo wa dhati ninakupongeza na ninaomba taasisi nyingine waige mfano katika Bunge ambapo miundombinu kwa watu wenye ulemavu imezingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali yangu mawili ya nyongeza. Nashukuru kwa majibu mazuri kwa Naibu Waziri na kwa Serikali pia. Kama alivyosema kwamba Serikali itaendelea kufuatilia kwa karibu suala hili, ninapenda kufahamu sasa ni lini basi utekelezaji wake utakamilika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; baadhi ya benki hapa nchini pamoja na kwamba zimejali mahitaji ya watu maalum, hasa walemavu wa viungo, lakini bado ramps zilizojengwa zina mteremko mkali ambao ni hatari zaidi kwa watu wenye ulemavu. Je, ni hatua gani sasa zinachukuliwa na Serikali kuhakikisha kwamba, ikiwa ni pamoja na kutoa maagizo kwa wafanyakazi au wahudumu wa benki kuwahudumia watu wenye ulemavu kwa kuwafuata nje na kuwapa huduma hiyo pale wanapofika katika benki hizo?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ameuliza ni lini basi utekelezaji utakamilika. Kama ambavyo nimesema kwenye jibu langu la msingi, Serikali tunaendelea kufuatilia na nimeeleza wazi kwamba miundombinu hii ina gharama kubwa, hasa hii yenye nuktanundu kwa ajili ya ndugu zetu ambao wana mahitaji maalum, hasa walemavu wa macho. Serikali tunaendelea kufuatilia kwenye mabenki yote ili kuhakikisha angalau katika ATM hizi wanafunga kwa uharaka mashine hizi ili kuwasaidia ndugu zetu waweze kupata huduma stahiki.

Mheshimiwa Spika, na hili alilolisema naomba nizielekeze benki zote nchini na naamini kwa Utanzania wetu, kwa utamaduni wetu tulivyolelewa Watanzania, huduma hizi zinatolewa, mtu mwenye ulemavu anapokuwa kafika benki kuhitaji huduma hizi watumishi wa benki zetu wamekuwa wakiwahudumia wakitoka nje kwenda kuwahudumia. Naomba tu nisisitize kwa zile benki na taasisi za kifedha ambazo hawajaanza kufanya huduma hizi basi waweze kuwahudumia ndugu zetu kutokana na uhitaji huo, nawaomba sana, na haya yachukuliwe kama maelekezo ya Serikali. Wakati huohuo benki zote kwenye miundombinu ya kuingia kwenye ATM ambapo wametengeneza step slopes basi warekebishe ili iwe rahisi kwa ndugu zetu wenye ulemavu kuweza kufikia huduma hizi kwenye mashine hizi.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya watu wenye ulemavu naomba niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa hivi karibuni kumekuwa na uhakiki wa simu, uhakiki wa passports zetu na shughuli za kibenki. Na kuna walemavu wengi ambao hawana vidole, na wanatumia vidole ili kuhakiki; je, Serikali imeweka mpango gani madhubuti wa kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki zao?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nimeipokea changamoto hii na ninaomba tufanye kazi kwa pamoja Wizara yetu ya Fedha, hasa kwenye taasisi zetu za kifedha na mabenki yetu na Wizara ya Uchukuzi na Mawasiliano ili tuone jambo hili tunalishughulikia kwa haraka na ndugu zetu hawa waweze kupata huduma hii.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, na inavyoonesha Benki ya Kilimo bado ina mahitaji ya mtaji mkubwa hasa ukizingatia kuwa kilimo kwa nchi yetu ndiyo tunakitegemea kwa kiasi kikubwa kwenye uchumi. Sasa ukiangalia katika jibu kwa Mkoa wa Mbeya ambayo imeoneshwa kuwa zimepelekwa shilingi milioni 700 lakini na hizi Wilaya alizozitaja Mheshimiwa Waziri siyo za Mkoa wa Mbeya ni za Mkoa wa Songwe. Kwa hiyo kwa jibu hilo inaelekea kabisa Mkoa wa Mbeya haujanufaika na mikopo ya Benki ya Kilimo.

Sasa swali langu; je, ni kwa kiasi gani Serikali imeweza kufanya tathmini ya mahitaji halisi ya mtaji wa Benki ya Kilimo? Na je, mtaji huo utapelekwa Benki ya Kilimo ukiondolea mbali hiyo mikopo ya ADB utapelekwa lini huo mtaji kwa Benki ya Kilimo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kiasi kikubwa ukiwapa wakulima mikopo risk kubwa iko kwenye bei kwa sababu bei za mazao hazieleweki, kuna risk sana kwenye bei. Sasa kwa kiasi gani Benki ya Kilimo kwa kutumia instruments za kibenki na vilevile kwa kusaidiana na taasisi zingine kama commodity exchange (TMX) zimeweza kutengeneza utaratibu wa kuondoa hiyo risk, wa ku-manage hiyo risk ambayo inatokana na changamoto za bei za mazao yetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza lenye (a) na (b), tathmini ya mtaji na utapelekwa lini; tathmini ya mtaji ilishafanyika na kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi tunaangalia njia nyingine za ku-finance benki yetu ya kilimo ili iweze kuwa na uwezo wa kuwakopesha wateja wake ambao ni wakulima wadogo, wa kati pamoja na wakubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu Bunge lako tukufu likafahamu kwamba mabenki yote hayakopeshi kupitia mtaji, yanakopesha kupitia njia nyingine, co-financing agreement, ndiyo maana Serikali ilitafuta mkopo wa bei nafuu kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika na ikaipatia Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania. Kwa hiyo, hilo naomba Waheshimiwa Wabunge tulifahamu; hakuna benki yoyote inayokopesha kupitia mtaji wake, inakopesha kupitia amana na njia nyingine za utafutaji wa fedha ili iweze kuwahudumia wateja wake. Serikali ipo tayari kabisa kuiwezesha benki yetu kupitia mipango mingine ili ipate fedha za kutosha za kuwahudumia wakulima wetu ambao ndio lengo kubwa la uanzishwaji wa benki hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la risk ya masoko; TMX ambalo ni Soko la Bidhaa Tanzania, limeanza kazi vizuri mwaka huu na tayari tumeona baadhi ya mazao kwa mfano ufuta ambao umetafutiwa soko zuri na Soko letu la Bidhaa Tanzania wameweza kutafuta masoko na sasa tunaendelea kutafuta masoko mengine kupitia Soko la Bidhaa Tanzania kwa ajili ya mazao yaliyobaki ili kuwasaidia wakulima wetu kuondokana na vihatarishi vya ukosefu wa bei au bei isiyoeleweka kwenye masoko yetu.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Namshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Amejieleza vizuri, tumeyaona kwenye karatasi hapo na yapo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, idadi ya watu katika nchi yetu inaongezeka na toka tumepata uhuru mwaka 1961 na Muungano 1964 tumeendelea kupambana na maadui watatu ambao ni ujinga, maradhi na umasikini. Angalau haya mawili ya maradhi na ujinga tunaelekea kuyamudu ndiyo maana idadi ya watu inaongezeka.

MWENYEKITI: Swali, swali!

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali; Serikali ina mpango gani sasa wa kupambana na adui namba moja ambaye ni umasikini unaoongezeka katika maeneo mengi hasa maeneo ya vijijini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kumekuwa na makundi makubwa ya vijana wanaohitimu elimu hasa Elimu ya Vyuo Vikuu. Sasa ndhi yetu ipo kwenye mkakati wa kujenga viwanda: Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwekeza katika viwanda vya Labor Intensive badala ya Capital Intensive ili kukidhi makundi makubwa ya vijana yanayohitimu shule na kwa sababu fursa tunazo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba umasikini ndani ya nchi yetu hauongezeki, unapungua kila mwaka. Hii naisema, siyo maneno yangu, ni maneno ya utafiti ambao umefanyika. Utafiti wa mapato na matumizi ya kaya binafsi uliofanyika mwaka 2018 na Mheshimiwa Waziri Mkuu akauzindua utafiti huu, unaonesha kwamba umasikini wa kipato umepungua kutoka asilimia 28.2 toka mwaka 2012 na sasa umefika asilimia 26.8 mwaka 2018. Hivyo siyo sahihi kuendelea kuimba wimbo wa Taifa letu kwamba watu wanazidi kuwa masikini. Siyo sahihi hata kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti huu pia unaonesha umasikini wa chakula kwa Watanzania katika kila kaya, mwaka 2012 ulikuwa asilimia 9.7; mwaka 2018 umasikini wa chakula kwa kaya ya kila Mtanzania ni asilimia 4.4. Kwa hiyo, tunaomba Watanzania wafahamu kwamba jitihada za Serikali yao na wao Watanzanzia wamejitolea kuelewa jitihada hizi za Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali yake wanafanya kazi kwa jitihada zote. Umasikini wa kipato na umasikini wa chakula umepungua kutokana na tafiti zilizofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili kwamba tuwekeze kwenye viwanda ambavyo vinatumia rasilimali watu zaidi kuliko kutumia capital intensive. Naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba katika viwanda ambavyo vimeanzishwa na vinaendelea kujengwa kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri wa uwekezaji asubuhi, ni viwanda vinavyotumia zaidi rasilimali watu. Viwanda hivi ni vile ambavyo vipo katika maeneo ya nguo. Tunafahamu hatujafanya vizuri zaidi, lakini jitihada zinaendelea kufanyika. Viwanda vya kutengeneza tiles havitumii mashine, vinatumia rasilimali watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vingine ni vya kuchakata mazao yetu, havitumii capital, vinatumia zaidi rasilimali watu. Nawaomba Watanzania wanaomaliza Vyuo Vikuu waweze kwenda kufanya kazi kwa tija kwenye viwanda hivyo.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Spika, haya ndiyo majibu ya muda mrefu, lakini anavyoanguka ndivyo anavyochinjwa. Nami nitakuja hivyo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Waziri, kwanza nakupongeza na miongoni mwa Manaibu Waziri wanaopigiwa simu wewe na Atashasta Nditiye mnapokea kwa wakati tofauti na Mawaziri wengine, hilo hongereni sana. (Makofi)

Mheshiniwa Naibu Waziri, swali hili limeulizwa karibu mara tano humu ndani nikiwemo mimi mwenyewe tarehe 6 Septemba, 2018 na leo ni tarehe 12 Septemba, 2019, ni mwaka mmoja na siku kidogo. Kama mwaka mmoja hivi tulifanyiwa semina hapa Ukumbi wa Msekwa, walikuja Ma-deputy governor karibu watano, Wakurugenzi na Watendaji na niliuliza swali hili, wakasema hizi fedha ziko Dutch Bank zitaletwa muda siyo mrefu. Sasa swali langu ni: Je, tokea muda huo zinaletwa kwa baiskeli ama kwa mguu? Maana ni muda mrefu hazijafika. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hivi juzi hawa jamaa walishinda kesi yao huko Uingereza: Je, ni kweli na kwamba waliambiwa waliofungua kesi hiyo walipe gharama za kesi? Ni kweli wameshinda kesi? Kama wameshinda, ni hatua gani zinazofuata? Wengine tukumbuke Mheshimiwa Naibu Waziri, cheo ni dhamana…

SPIKA: Maswali yasiwe mengi, nataka maswali mawili tu Mheshimiwa Jaku.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza, amekuwa mfuatiliaji mzuri sana tangu benki hii ilipofutiwa usajili wake hapa nchini akifuatilia amana za wateja ili waweze kulipwa. Kwa dhamira njema na nia njema ya Serikali yetu, ndiyo kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba kwa shilingi milioni 1.5 wateja ambao walikuwa na amana hiyo ndani ya benki, yatari tumeshalipa zaidi ya asilimia 83 ya wateja wote. Asilimia 17 iliyobaki ni wateja ambao hawajajitokeza wao wenyewe kuja kuchukua amana zao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba dhamira ya Serikali yetu ni njema na ndiyo maana tumeanza kulipa hawa wateja wote ambao walikuwa na fedha zao ambazo hazizidi shilingi milioni 1.5 kama sheria inavyotuelekeza.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la kwanza naomba niyajibu yote mawili kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza fedha hizi hazitakuja kwa baiskeli, wala kwa gari, wala kwa meli, ila ni taratibu za kisheria zitakapokalimika. Nachukua fursa hii kumpongeza sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wakili Mkuu wa Serikali pamoja na Benki Kuu ya Tanzania, wanafanya kazi kubwa kuhakikisha amana za wateja wetu wote ambao wako ndani ya Tanzania na nje ya Tanzania zinabaki kuwa salama na wanazipata pale ambapo tumemaliza majadiliano na Benki Kuu ya Cyprus.

Mheshimiwa Spika, tayari mwezi wa Tisa baada ya Mahakama za nchini Cyprus kurejea na kuanza kufanyakazi yao, kesi zote zilizokuwa zimefunguliwa, tumekubaliana zitafutwa na tayari sasa fedha hizo zitafika ndani ya nchi yetu na watu wetu wote wataweza kulipwa fedha zao.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, naomba tu nitoe majibu ya nyongeza kwa swali la nyongeza alilouliza Mheshimiwa Mbunge na hasa kuhusu ile kesi ya Uingereza.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wamiliki wa iliyokuwa Benki ya FBME walifungua kesi Uingereza. Lakini lengo la kesi ile ilikuwa ni ku-challenge mwenendo wa mchunguzi aliyekuwa anachunguza masuala ya FBME kule Uingereza, ni kweli kwamba Mahakama kule imetoa hukumu yake lakini kwa namna yoyote hukumu au matokeo ya kesi ile haiathiri suala zima la liquidation ya ile benki huku. Kwa maneno mengine, hukumu ile haina athari yoyote wala haigusi jambo lolote katika mchakato unaoendelea kwa upande wa Tanzania na Cyprus.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa benki hii ilikuwa na matawi Dar es Salaam, Mwanza na Arusha, na kwa kuwa benki hii ilikuwa na wafanyakazi zaidi ya 100 na familia hizo na wafanyakazi hao mpaka sasa hawajui hatma yao, familia hizo zinateseka kulipa ada, kulisha ndugu na kadhalika.

Je, ni lini sasa wafanyakazi hao watafahamishwa hatima yao kwa sababu pia hawawezi hata kwenda kuomba kazi mahali pengine popote?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimesema kwenye majibu ya msingi na majibu ya nyongeza ambayo nimemjibu Mheshimiwa Jaku Hashim, baada ya kuwa tumemaliza majadiliano na Benki Kuu ya Cyprus na kuingia sasa kwenye mchakato wa kuhakikisha kila mwenye haki yake anapata haki yake ni imani yangu na wafanyakazi hao wa iliyokuwa Benki ya FBME Limited watapata haki yao, nimesema wazi mwezi wa Septemba, baada ya Mahakama za nchini Cyprus kurejea kazini basi yote hayo yatajulikana na kila mmoja atapaa haki yake na kwa wafanyakazi kwa sababu waliajiriwa na Benki hii ambayo ilikuwa na Makao Mkuu hapa nchini, basi sheria zetu za kazi na ajira zitatumika ili kila mtumishi aweze kupata haki yake.(Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuruku, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza, Mheshimiwa Waziri uko tayari kunipatia mchanganuo wa hao wafanyakazi 7,000 wanaohitajika wanatosheleza kwa kiwango gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Swali langu la pili, kwa kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania ndiyo mamlaka iliyopewa wajibu mkubwa wa kukusanya kodi; na kwa kuwa ukirejea hotuba mbalimbali za Wizara ya Fedha utaona kuna upungufu mkubwa sana wa wafanyakazi; na kwa kuwa huko mtaani kuna vijana wengi ambao wamehitimu kwenye masuala mbalimbali ya kodi lakini hawajaajiriwa. Sasa nataka kujua, ni lini Serikali itaajiri Vijana wale ili wapate ajira na Mamlaka ifanye kazi kwa ufanisi kwa maendeleo ya taifa hili? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza, anasema nimpatie mchanganuo wa hao watumishi 7,000. Mheshimiwa Tunza nimesema wanaohitajika ni 7,000 ambao tulionao Watumishi walioajiriwa ni 4,751 hawa hata leo hii nikimaliza kujibu maswali haya niko tayari kukupatia hawa 4,751. Kwa hao 7,000 pia niko tayari kukuandalia mchanganuo huo kwa kada zote ambazo zinahitajika na kukupatia ikiwezekana siku ya jumatatu tuwasiliane na nikupatie mchanganuo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, naomba kwanza niseme, si kwamba Mamlaka ya Mapato ina upungufu mkubwa wa watumishi kama alivyosema, upungufu uliopo ni wa asilimia 28 tu siyo upungufu mkubwa. Kwa hiyo kama nilivyosema tunahitaji 7,000 tulionao ni 4,751 na Serikali ya Awamu ya Tano imejitahidi kwa kiwango kikubwa; tangu imeingia madarakani tayari tumeshaajiri Watumishi 692 na kwa mwaka huu tayari kwenye Bajeti yetu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania tutaajiri watumishi 150. Kwa hiyo tunakwenda hatua kwa hatua mpaka mwisho tutakamilisha wote Watumishi 7,000 wanaohitajika ili kuhakikisha Mamlaka ya Mapato Tanzania inafanya kazi zake kwa ufanisi.
MHE. LUCY S. MAGERELI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Baada ya maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, natamani kufahamu, Serikali inafanya jitihada gani na kwa kutumia utaratibu gani kuhakikisha kwamba watumiaji wa huduma ndogo za fedha wanapata taarifa kuhusu hii sheria mpya, lakini hizi kanuni ambazo amezitunga pamoja na hiyo grace period ambayo wamewapa kabla ya kaunza utaratibu wa usajili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika majibu yake anasema lengo la kutungwa sheria hii ilikuwa ni kutatua changamoto ikiwemo ya utozaji wa riba kubwa lakini suala la utozaji wa riba kubwa si tu kwa sekta ndogo ya fedha hata huduma za fedha kwa ujumla wake kwa maana ya sekta rasmi kwa maana ya mabenki bado riba zinazotozwa ni kubwa sana. Je, Serikali inafanya nini kuhusu hili la ku-regulate hata riba ambazo zinatozwa na mabenki sasa hivi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Lucy Simon Magereli, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza jitihada na utaratibu ambao Serikali tunatumia kufikisha taarifa ni kwamba tunaendesha makongamano sehemu mbalimbali, ndiyo maana kwenye jibu langu la msingi nimesema kwamba tumewashirikisha walengwa wote katika katika makundi yote manne yaani kuanzia tier one to tier four, wote wameshirikishwa tulipokuwa tunaandaa kanuni hizi za ujumla za Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Pia kanuni maalum kwa ajili ya daraja la pili mpaka daraja la nne, tumekaa na makundi mbalimbali, tumeendesha semina na warsha mbalimbali. Tunapokamilisha kuandaa kanuni hizi ambazo tayari zimeshatolewa tarehe 2 Agosti, tutaendelea kuwatembelea wenye taasisi hizi ili tuweze kuwafikia kwa ujumla na wawe na uelewa wa pamoja wa dhamira njema ya kuandaa Sera yetu ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 pamoja na sheria yake ya mwaka 2018 na kanuni zake zote mbili za mwaka 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, naomba kumwambia Mheshimiwa Lucy kwamba riba inayotozwa katika sekta rasmi ya taasisi za fedha siyo kubwa. Nakumbuka wakati tulipoingia madarakani mwaka 2015, riba ilikuwa kuanzia asilimia 21 hadi asilimia 25, lakini kwa sasa katika taasisi ambazo ni rasmi za kifedha, pamoja na jitihada kubwa zilizochukuliwa na Benki Kuu ya Tanzania ya kushusha discount rate pamoja na amana inayotakiwa kuwekezwa Benki Kuu, riba ni kuanzia asilimia 15 hadi asilimia 17.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba mabenki haya au taasisi hizi za fedha wanapo-set riba hii, huwa wanaangalia mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na gharama wanazozitumia katika kutoa huduma hizi. Serikali tunajitahidi sana kusimamia taasisi hizi za kifedha ili kuhakikisha eneo moja ambalo lilikuwa likichangia riba kuwa juu nayo ni administration inakwenda chini, administrative cost ishuke ili riba iendelee kushuka kwa faida ya Watanzania na uchumi wetu kwa ujumla.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ninasikitika sana kwa majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, tulipoomba Serikali itoe kodi na ikakubali ilikuwa ni furaha kwa Wanawake wengi wa Nchi hii ya Tanzania. Jana ilikuwa ni siku ya hedhi salama kwa wanawake duniani. Tumeonana na wadau wanaoshughulikia pads, hakuna lalamiko walilolitoa juu ya uendeshaji zaidi ya kodi ambayo Serikali imetoa kwa wanao- import na kuwaacha watengenezaji waliko hapa nchini.

Swali langu; ni nini Serikali itafanya kuweza kusaidia wawekezaji wa ndani wanaotengeneza taulo hizi ikiwemo Jessy, HQ na wengineo ili kuweza kupunguza gharama ya taulo za kike?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali itakubali kuweka ulazima wa wauzaji wanaouza taulo hizi kuweka gharama ya bei katika taulo hizo ili kufanya bei zote zifanane kama ilivyo kwa mazao kama ya Coca cola na Pepsi nchi nzima ina bei moja. Serikali itachukua wazo letu la kuona wkamba ni lazima iandikwe bei katika taulo hizo ili kukwepa kwa wale wanaoweza kuongeza hasa wasafirishaji na wauzaji na bei hii iweze kupungua.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kusahihisha alichokisema kwamba wazalishaji wa ndani bado wanalipa kodi ya ongezeko la thamani kwenye bei ya bidhaa hizi, hapana. Tumeondoa kodi ya ongezeko la thamani kwenye bidhaa hii kwa bidhaa zinazotoka nje ya Nchi na zile zinazozalishwa ndani ya Nchi ndiyo maana nikasisitiza kwenye jibu langu la msingi, majibu ambayo Serikali iliyatoa kwa swali namba 2938 ambalo liliulizwa na Mheshimiwa Stella Ikupa Allex na kwa mwongozo wako naomba kulisoma swali lake liliuliza hivi:-

“Kutokana na umuhimu wa taulo za kike Nchini, Je, Serikali inaonaje ikiondoa kodi kwenye taulo hizi?”

Mheshimiwa Spika, Serikali ilisema kwenye swali hili kwamba ukiondoa kodi haiwezi kuleta atahari moja kwa moja kwenye bei ya bidhaa husika kwa sababu bidhaa husika inategemea mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, tukienda Nchini Botswana, tukaenda Nchini Kenya ambako waliwahi kuondoa kodi kwenye bidhaa hizi hakuna athari yoyote iliyoonekana kwenye taulo hizi za kike. Kama tunataka kweli kumsaidia mtoto wa kike kama kweli tuna dhamira ya dhati ya kumsaidia mtoto wa kike, naomba tuisikilize Serikali inasema nini; Serikali siku zote imekuwa ikisisitiza kwamba, sisi kama Serikali tuna mpango na tayari tumeanza kufanya mchakato wa kuona ni jinsi gani ya kutoa bidhaa hii bure kwa watoto wa kike na siyo kuondoa kodi jambo ambalo halina athari yoyote zaidi ya kupunguza mapato ya Serikali. Jambo hili lilipelekwa kisiasa zaidi na mimi nawaomba kwenye mambo ya msingi yanayogusa Watanzania tusiingize siasa, hilo ndiyo suala ambalo nataka kuliweka hivyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili baada ya majibu yangu haya ya swali lake la kwanza, hakuna ulazima wowote wa kuandika bei kwenye bidhaa hizi kwa sababu tuko kwenye soko huria na Serikali yetu hatutaki kuingilia jambo hili, tunachohitaji ni kuja na mpango wa kibajeti wa ku-deal na jambo hili ili tuwasaidie watoto wetu wa kike.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda nimuulize Mheshimiwa Waziri, umekuwepo utaratibu wa Waafrika wote, kutoka nchi mbalimbali wanapotaka kuja ndani ya Tanzania na usafiri wao binafsi wanaingia kwa kupata permit katika mipaka yetu. Je, ni kwa nini Wazanzibar ambao wanataka kuingia na magari yao Tanzania Bara kwa ajili ya matumizi na kurudi Zanzibar, hawapati ruhusa hiyo na badala yake wamekuwa wanawekewa vikwanzo kuingia na magari yao kwa matumizi binafsi na baadaye kurudi nayo Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Khatib, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, amesema vizuri Mheshimiwa Khatib lakini angetusaidia pia kama hata yeye wakati ameingia Tanzania Bara na gari lake alipewa permit kwa ajili ya kuendesha gari lake hilo huku Tanzania Bara?

Mheshimiwa Spika, niliambie Bunge lako Tukufu kwa nini tuko katika mkanganyiko huo. Siku zote naposimama hapa nimekuwa nikisema kwamba Mamlaka ya Mapato Tanzania Bara na Mamlaka ya Mapato Tanzania Visiwani wanatumia mifumo tofauti ya uthaminishaji wa mizigo. Ndiyo maana magari yanapopita Zanzibar kuja huku Tanzania Bara lazima yafanyiwe uthamini upya ili kujiridhisha na kodi ambayo imelipwa ili kuleta fair competition kwenye biashara zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hilo linafahamika vizuri na nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kutoka Zanzibar wengi wao katika hili hawakubaliani. Kwa hiyo, niombe tuweze kukubaliana kwenye jambo hili ili tuondoke kwenye mkanganyiko huu na tuweze kuwahudumia watu wetu vizuri.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza swali la nyongeza, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nakumbuka mwaka 2017/2018 Serikali ilitenga karibuni bilioni 900 kwa ajili ya shughuli za maendeleo kwenye Wizara ya fedha, na fedha hizi, zilikuwa zinakwenda kutoa elimu kwa walipa kodi watanzania, na sasa hivi kumekuwa na kero kubwa sana ya kodi kwenye nchi hii, na biashara nyingi zinafungwa katika Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, Je, Serikali imejipanga namna gani, namna ya kutoa elimu kwa walipa kodi ili Watanzania hawa waweze kujua wanalipa kodi kutoka kwenye faida, au wanalipa kodi kutoka kwenye mtaji? Kwa sababu elimu hiyo hawana mpaka sasa hivi, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwenye jibu langu la msingi, nimeelezea Elimu ya Kodi hutolewa katika ngazi mbalimbali, kuanzia ngazi ya Taifa Mamlaka ya Mapato Tanzania hukaa na Wafanyabiashara kuwapa Elimu ya Kikodi physically yaani uso kwa uso lakini pia kupitia Vyombo mbalimbali vya Habari.

Mheshimiwa Spika, lakini pia hata sisi Viongozi Wakuu wa Wizara ya Fedha tumekuwa tukizunguka katika Mikoa mbalimbali kukutana na wafanyabiashara na kupeana Elimu ya Kikodi tukiwa na Wataalamu wetu wa Kikodi. Lakini pia kila mwezi Wakuu wa Mikoa huwa na Mabaraza ya Biashara kwenye Mikoa yao, hukutana na wafanyabiasha na kutoa Elimu ya Kikodi Wataalamu wetu wa Kikodi wanakuwepo.

Vilevile Wakuu wa Wilaya wana Mabaraza ya Biashara ya Wilaya ambapo hukutana na wafanyabiashara, wataalam wetu wa Kodi wakiwepo na Elimu ya Kikodi hutolewa.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito kwa Watanzania, kwa Wafanyabiashara wote kuchukua jukumu la kuhudhuria Mikutano hii ili waweze kupata Elimu ya Kikodi na kero zao mbalimbali za Kikodi ziweze kutatuliwa.

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Mwakajoka amesema biashara nyingi zimefungwa, hili ni suala ambalo linaongelewa katika ujumla wake, nilishaliambia Bunge lako Tukufu kufungwa na kufunguliwa kwa Biashara ni jambo la kawaida katika Mataifa yote Duniani, siyo kwa Tanzania peke yake, na nilishaeleza, rate ya Biashara kufungwa ni ndogo kuliko rate ya Biashara zinazofunguliwa, nashukuru sana.
MHE. RUKIA AHMED KASSIM: Mheshimiwa Spika, ahsante, nami kunipa nafasi ya kuweza kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha swali la nyongeza, nilitaka kujua kwa sababu Mbunge ana haki ya kuleta gari yake kwa kupitia exemption kama Mbunge, ana haki ya kuileta Tanzania Bara au Tanzania Visiwani. Ni kwani basi anapoleta gari yake Tanzania Visiwani, akiileta Bara hawezi kupewa namba ya hapa mpaka anaambiwa ailipie difference? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nimeshaeleza changamoto ya Kimfumo tuliyonayo, unapopewa namba ya Tanzania Bara, maana yake gari ile inasajiliwa kutumika Tanzania Bara, kwa hiyo, kama inasajiliwa kutumika Tanzania Bara na utofauti wa Kimfumo nilioueleza ni lazima tuweze kuthaminisha gari yako sasa inasajiliwa Tanzania Bara tukupe namba ya Tanzania Bara na uweze kulipia utofauti ule wa Kodi uliopo kwa sababu ya mfumo wetu wa utofauti kati ya Mamlaka mbili hizi ili gari lako liweze kutumika Tanzania Bara.
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Serikali kudhibiti makampuni haya haramu kufanya biashara hii, ila yamekuepo baadhi ya makampuni haya yanayoendesha biashara hii kinyume na sheria. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia waathirika ambao fedha zao zimetapeliwa katika makampuni haya? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; waathirika wakubwa wa biashara hii ni akina mama na vijana kutokana na mikopo yenye riba kubwa kwa mabenki, je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia vijana na akinamama kuwapa mikopo yenye riba nafuu ili kuepukana na biashara hii haramu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza, kuwasaidia waathirika wa fedha hizi. Napenda kuliambia Bunge lako tukufu kwamba washiriki wa biashara hii haramu wote, yule anayewashajihisha watu kufanya biashara hii na wale wanaoshiriki biashara hii wote wameshiriki kwenye biashara haramu kutokana na Sheria ya Makosa ya Jinai kama nilivyotaja kifungu 171A, B na C, wote wawili wanatenda kosa na wote wawili hawatakiwi kusaidiwa chochote zaidi ya kupata adhabu ya kushiriki katika biashara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili; ni vipi Serikali inawasaidia vijana na akina mama; kwa dhamira njema kabisa Serikali yetu ilileta sheria hapa ya microfinance, Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha mwaka 2018 ambapo kanuni zake zinakamilika na zitaanza kutumika kuanzia tarehe 1 Julai, 2019 ili kuhakikisha vijana na akina mama wanapata mikopo kutoka kwenye taasisi halali ambazo zinatoza riba yenye kulipika, riba ambayo ni nafuu kabisa kwa vijana wetu na akina mama.

Lakini pili, Serikali yetu kupitia Bunge lako tukufu mwaka 2018 ilipitisha mabadiliko ya sheria kwenye Sheria ya Fedha kuhakikisha asilimia kumi ya mapato ya ndani ya Halmashauri inakuwa sasa ni lazima na ni sheria kwa Wakurugenzi wote wa halmashauri kutoa asilimia kumi hii na asilimia kumi hii ya mikopo inapotolewa haitozwi riba yoyote, riba yake ni sifuri ili akina mama na vijana wapate fedha hii waweze kufanya biashara zao bila kulipa riba yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia chini ya Wizara ya Fedha na Mipango tuna Taasisi ya Self Microfinance Bank ambayo inatoa mikopo katika riba nafuu sana kwa akina mama na vijana na imefanya vizuri katika mikoa mbalimbali. Naomba niwaombe na niwatake vijana wetu na akinamama wasijihusishe kwenye biashara haramu ila waende kwenye taasisi ambazo ni halali zenye dhamira njema ya kujenga uchumi wa taifa letu.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya ngongeza.

(a) Ni kwa nini sasa fedha za Wahisani zinachelewa kufika kwa wakati na nyingi zinakuja wakati tunamaliza mwaka wa fedha?

(b) Naomba sasa Serikali itoe orodha ya nchi wahisani ikionesha mwenendo wa walichochangia katika kipindi cha miaka mitatu ya fedha iliyopita?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Washirika wa Maendeleo hutoa fedha kulingana na makubaliano ya kimkataba yaliyopo kati ya Serikali na washirika hao. Kwa kutambua hilo, baadhi ya Washirika wa Maendeleo hutoa fedha mwishoni mwa mwaka wa fedha wa Serikali kutokana na kupishana kwa kalenda kati ya mwaka wa fedha wa Serikali na kalenda za mwaka wa fedha wa Washirika wa Maendeleo, jambo ambalo Serikali hulizingatia katika mipango yake.

Hivyo basi, siyo kweli kwamba fedha za wahisani zinachelewa kufika kwa wakati. Fedha hizo hutolewa kwa mujibu wa mikataba hiyo ambayo inaainisha muda ambao Washirika wa Maendeleo wanatakiwa kutoa fedha hizo ili kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopangwa kutekelezwa na Serikali.

(b) Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita (2016/2017 – 2018/2019), Serikali imekuwa ikipokea fedha za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kutoka kwa nchi wahisani kwa kiwango cha kuridhisha kutoka kwa nchi wahisani pamoja na Washirika wa Maendeleo wakiwemo Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Afrika, Umoja wa Ulaya, Japan, Korea, India, Finland, Ufaransa, Ujeruman, Global Fund, IFAD, Norway, Umoja wa Mataifa (UN) pamoja na Sweden.

Aidha, orodha ya nchi wahisani pamoja na Washirika wa Maendeleo ikionesha mwenendo na kiasi walichochangia kwa kipindi hicho tutaiwasilisha kwa Mheshimiwa Mbunge baada ya kufanya uchambuzi wa kina kama alivyoomba.