Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Joyce John Mukya (1 total)

MHE. JOYCE J. MUKYA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la maji katika Mkoa wa Arusha?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joyce John Mukya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika kutatua tatizo la maji Jiji la Arusha imepata mkopo wa Dola za Marekani milioni 210.96 sawa na shilingi bilioni 462.37 kutoka Benki ya Maendeleo Afrika (AFDB-African Development Bank) ili kutekeleza mradi wa upanuzi wa mtandao wa maji safi na maji taka sambamba na kuboresha vyanzo vya maji. Mradi huu mkubwa utawezesha Jiji la Arusha pamoja na viunga vyake ikiwa ni pamoja na vijiji vyote vilivyopo umbali wa kilometa 12 kandokando ya bomba kuu kupata huduma ya maji safi na maji taka. Jumla ya gharama za ujenzi ni Dola za Marekani milioni 233.92 sawa na shilingi bilioni 512.69.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Arusha, imeshapata Mhandisi Mshauri wa kupitia usanifu ikiwa ni pamoja na kuandaa makabrasha ya zabuni. Kazi ya ujenzi inatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka wa fedha 2006/2007 hadi 2025, Serikali itatekeleza Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji yenye lengo la kuhakikisha kuwa kila mwananchi anapata huduma ya maji safi na salama. Katika mpango wa miradi ya maji ya Vijiji 10, Mkoa wa Arusha unatekeleza jumla ya miradi 71 katika halmashauri zote saba ambapo miradi 19 imekamilika na inatoa huduma ya maji kwa wakazi wapatao 112,412. Miradi 52 iko katika hatua mbalimbali za ujenzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanzisha Mfuko wa Maji ambao utasaidia kuondoa tatizo la upatikanaji wa fedha na hivyo miradi itatekelezwa kama ilivyopangwa. Lengo la Serikali ni kukamilisha miradi yote inayotekelezwa katika Halmashauri zote za Mkoa wa Arusha ili kuhakikisha wananchi wanapatiwa huduma ya maji safi.