Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Joram Ismael Hongoli (44 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kushukuru kwa kupewa nafasi hii nami kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Rais ya tarehe 20 Novemba, 2015. Nimshukuru kwanza Mwenyezi Mungu kwa yote aliyonijalia mpaka leo hii nikaweza kuwepo mahali hapa. Lakini pili, niwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Lupembe kwa imani kubwa waliyoiweka juu yangu mimi wakanichagua na kuwawakilisha katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Rais ni nzuri sana na kwa kupitia hotuba hii wananchi wa Jimbo langu la Lupembe na wananchi wote wa Tanzania wameifurahia sana, kwani inaonyesha mwelekeo mzuri na matumaini mazuri ya kimaendeleo hasa kiuchumi lakini pia maendeleo ya jamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba yake Mheshimiwa Rais ya tarehe 20 Novemba alieleza sana juu ya viwanda hasa viwanda vidogo vidogo ambavyo vinaajiri watu wengi sana. Viwanda hivi vimekuwa vikiajiri watu wengi na hivi viwanda ni vile viwanda vinavyohusika sana na usindikaji wa mazao mbalimbali kwa ajili ya kuongeza thamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Lupembe tuna kiwanda cha muda mrefu sana, Kiwanda cha Chai Igombola ambacho hivi sasa ninavyoongea kwa takribani miaka zaidi ya nane kiwanda hiki kimefungwa, kilifungwa tarehe moja mwezi wa nane mwaka 2008, kutokana na mgogoro uliokuwepo kati ya Wakulima na Mwekezaji. Naomba Serikali ijitahidi au ifanye jitihada za kuhakikisha kwamba kiwanda hiki kinafunguliwa ili wananchi wale wa Lupembe waweze kuuza mazao yao ya chai, lakini pia tuweze kuimarisha uchumi na hatimaye Serikali ikaweza kukusanya kodi kutokana na mishahara ambayo itatokana na wafanyakazi watakaokuwa wameajiriwa pale, lakini pia iweze kupata tozo kwa maana ya kodi kwenye kiwanda kile na hatimaye kuweza kuinua uchumi wa wananchi wa Lupembe ambao umezorota sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichukue nafasi hii kuelezea kidogo juu ya zao letu la chai. Zao hili limekuwa likilimwa maeneo yangu na ndiyo zao kuu tunalolitegemea sana sisi wana Lupembe. Lupembe ipo Halmshauri ya Wilaya ya Njombe, mnafahamu wote ni Halmashauri ya zamani sana hii, na Lupembe ilikuwa ni miongoni mwa maeneo hapa nchini yanayoongoza kwa ulimaji wa chai. Lakini zao hili la chai limekuwa likiuzwa kwa bei ndogo sana ukilinganisha na bei za uzalishaji wa zao hili. Sasa hivi linauzwa kwa shilingi mia mbili hamsini lakini bei ya uzalishaji, gharama za uzalishaji, ukijumlisha zote za kuuzia, gharama za uzalishaji wa kilo moja ya chai ni shilingi 450/=. Kwa hiyo wakulima hawa wanafanya hiki kilimo kwa hasara.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Serikali iweze kuziangalia kodi mbalimbali ambazo zimeingizwa kwenye zao hili ili ziweze kupungua na hatimaye wakulima wa Lupembe waweze kupata faida kutokana na zao hili la chai.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niweze kuongelea kidogo juu ya elimu, tumesema kwamba Serikali hii sasa kwanza wananchi wangu wamefurahi baada ya Mheshimia Rais kutangaza kwamba sasa elimu ni bure. Kwa hiyo, wananchi wengi waliokuwa wanashindwa kupeleka watoto wao shule sasa wataweza na wameshaanza kupeleka kwa wingi sana. Lakini kupeleka wanafunzi wengi haisaidii kama hatujatengeneza mazingira mazuri kwenye shule hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu moja wapo niiongelee kidogo ni kuhusu walimu hususani madaraja ya walimu, upangaji wa madaraja ya walimu ya mishahara, kumekuwa na tatizo kubwa sana, walimu wamekuwa wakilalamika. Utakuta kwa mfano, mwalimu amefanya kazi miaka saba, nane akiwa na level ya diploma anaenda kusoma degree, anaporudi anapewa daraja lile la “D” halafu anapewa daraja bila kupewa mshahara. Tunaita anapata dry promotion, sasa dry promotion zimekuwa zikikatisha sana tamaa kwa walimu kufanyakazi. Kwa hiyo, tusipoboresha kwenye upande wa walimu hasa madaraja wanapopata promotion ni vizuri yaendane na malipo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika sasa hivi utakuta kwamba mwalimu anaporudi kutoka chuoni kwenda kufundisha wakati alikuwa amefanya kazi muda mrefu anaenda kuanza ngazi ya mshahara sawasawa na yule kijana au mwanachuo anayeanza kazi. Sasa hii inawakatisha tamaa walimu wengi sana na ndiyo maana utakuta tunasomesha walimu wengi lakini mwisho wa siku walimu wanaamua kuhama kada wanahamia kada nyingine, kwa kuwa wanaona kada hizi za walimu kidogo zinausumbufu na maslahi yake yapo duni. Naomba Serikali iangalie uwezekano wa kurekebisha utaratibu huo, mimi naamini kwamba ingekuwa ni vizuri kama mwalimu amefanya kazi ameenda kusoma anaporudi basi angalau aongezee ngazi ya mshahara nzuri zaidi kuliko wale wenzake waliobaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, ilivyo sasa hivi utakuta kwamba wenzake waliobaki ambao hawajaenda kusoma wanakuwa na mshahara mkubwa zaidi, wanapewa daraja zuri zaidi kuliko yule aliyeenda kusoma. Kwa hiyo, kwa kada ya walimu kusoma sasa imekuwa kama ni adhabu. Tunaomba Serikali iweze kurekebisha jambo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niseme kidogo juu ya huduma ya afya. Jimbo langu la Lupembe ambayo ndiyo Halmashauri ya Wilaya ya Njombe mpaka leo hii haina hata hospitali moja na mpaka leo hii ina kituo cha afya kimoja, Halmashauri nzima, Jimbo zima na zahanati ndogo ndogo na vituo vya afya vingine viwili ambavyo bado vipo kwenye ujenzi. Wananchi wale wanapata shida sana ili waweze kujifungua hasa kwa operation kuna baadhi ya wananchi wanatembea kilometa mia moja arobaini na saba kwenda kutafuta Hospitali ya Kibena ili waweze kupata operation za uzazi. Naomba Serikali ijaribu kuliona hili jambo la muhimu sana tunaomba tupewe hospitali ya Wilaya lakini pia vituo vyetu hivi vitatu viweze kuboreshwa viwe na huduma ya operation kwa maana ya theatre ili akina mama wasiteseke kutembea umbali mrefu na wengine kupoteza maisha kwa sababu ya kukosa huduma ya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kidogo juu ya wastaafu. Wastaafu waliostaafu kuanzia mwezi wa sita mpaka mwezi Disemba hawajalipwa mafao yao wanataabika huko, wanalalamika na wanailaumu Serikali. Kwa hiyo tunaomba Waziri mwenye dhamana aweze kuchukua jitihada ya kuhakikisha kwamba hawa wastaafu wetu waliofanya kazi muda mrefu, waliojenga Taifa hili wanapata mafao yao haraka ili waendelee kuishi vizuri na kufurahia kustaafu kwao.
Mheshimiwa Naibu Spika, niongee kidogo juu ya jambo moja kuhusu umeme, Jimbo langu Halmashauri ya Wilaya ya Njombe sehemu kubwa halina umeme. Tuna vijiji 49 lakini vijiji tisa tu ndivyo vyenye umeme. Namuomba Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana na sisi pia atufikirie kule kijijini tuweze kupata huduma ya umeme ili tujisikie na sisi ni miongoni mwa Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niongee jambo kidogo kuhusu maji. Katika Jimbo langu la Lupembe na ndiyo Halmashauri ya Wilaya ya Njombe vijiji vingi havina maji, mpaka sasa hivi ni vijiji nane tu ndivyo vyenye maji. Sasa kwa hali hii ndugu zangu au Serikali tunaomba mtuangalie na sisi tupate maji kama alivyosema Rais hii Serikali ni Serikali ya kuwatua kina mama ndoo ya maji, basi mtutue na sisi kule Wanalupembe na sisi tujisikie kwamba wake zetu, mama zetu, wanafurahia maisha kwa kutuliwa ndoo za maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nisema kidogo juu ya Halmashauri yetu ya Wilaya ya Njombe ipo kwenye Halmashauri nyingine, ipo kwenye Halmashauri ya Mji wa Njombe. Sasa Watendaji wengi na wananchi wengi wanapata shida sana kupata huduma na ile ni Halmashauri Mama ni Halmashauri ya zamani sana. Sasa hivi ukienda hakuna hata gari moja……
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hongoli muda wako umekwisha.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kushukuru kwa kupewa nafasi hii, lakini pia namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuwasilisha Mpango mzuri ambao unaonesha mwanga wa maendeleo katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kwamba, ili tuweze kuendelea na kufikia uchumi wa kati, tunahitaji mipango mizuri kama ilivyooneshwa kwenye Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2016/2017 na 2016 - 2020. Katika Mpango huu kuna sehemu moja ambayo nitaiongelea sana hasa miundombinu ya barabara. Ili tuweze kuendelea kama nilivyosema, ni lazima tuwe na barabara nzuri ambazo wakulima wengi wanazitegemea, lakini pia hata viwanda vinategemea barabara au miundombinu. Barabara nyingi zinazokwenda vijijini ambako ndiko tunakoweza kupata malighafi za kuendeshea viwanda vyetu ambavyo tunasema kwamba tunataka tuingie kwenye uchumi wa viwanda, ni mbaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapokuwa na barabara nzuri, tunapokuwa na barabara za lami inakuwa rahisi kwa wakulima hawa kuweza kusafirisha mazao yao ambayo ndiyo malighafi za viwanda na hatimaye wakaweza kuuza mazao yao kwa haraka zaidi na yakapata bei nzuri zaidi; lakini siyo bei tu, hata ubora wa mazao yao na ubora wa bidhaa ambazo zitatokana na haya mazao zitakuwa bora zaidi na hatimaye kuweza kupata faida kubwa au kupata products ambazo zinaweza kuuzwa hata nchi za nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ilivyo sasa hivi, products zetu nyingi zinakataliwa, haziwezi kupata soko la nje kwa sababu tu hazina ubora na inaonekana kwamba ubora huu unakosekana kwa maana ya kwamba bidhaa nyingi zinafika kiwandani zikiwa zimechelewa au zimeharibika. Kwa mfano, kama bidhaa za matunda, zinafika kiwandani zikiwa zimeharibika. Kwa hiyo, hata zao lake au lile zao linalokuja kutoka kiwandani linakuwa halina ubora na hatimaye zinakataliwa kwenye masoko mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba pia Mpango uweze kuboresha miundombinu ya barabara. Kwa mfano, katika maeneo ya uzalishaji, mimi natoka Jimbo la Lupembe ambapo sehemu kubwa tunazalisha chai, lakini tunazalisha matunda, mananasi, tunazalisha matunda mengine kama parachichi na mengineyo. Barabara za kule hazipitiki kwa hiyo, wakulima wanashindwa kuuza mazao yao.
Mheshimiwa Waziri hasa Waziri wa Ujenzi, ukienda kuangalia jinsi gani wananchi wanavyomwaga haya mazao, jinsi gani chai inavyomwagwa kila siku, utawaonea huruma na utatamani kulia. Kwa hiyo, tuombe miundombinu hasa ya maeneo haya ambayo yana uzalishaji mkubwa, barabara zitengenezwe vizuri ili hatimaye wananchi waweze kuuza mazao yao na hatimaye kupata faida na kama Taifa kuweza kuongeza uchumi wa nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zetu kwa mfano nikisema hii ya Lupembe, ilishaingia kwenye ilani ya mwaka 2010 kwamba itatengenezwa kwa kiwango cha lami na mara moja kwenye Bunge la Bajeti fedha zilishakadiriwa kwamba tutapewa, lakini fedha hazikutoka. Nashangaa mwaka huu pia sijaiona kwenye Mpango kama itaaanza kutekelezwa hasa huu Mpango wa mwaka 2016/2017 wakati tayari ilishaahidiwa kwamba hii barabara itatengenezwa kwa kiwango cha lami.
Kwa hiyo, nakuomba Waziri wa Ujenzi nafikiri unanisikia vizuri sana na ni msikivu, hebu tujaribu kuingiza au tuingize kwenye Mpango ili sasa mazao haya ya chai na chai ya Lupembe mnaifahamu ni chai bora na ilikuwa ni moja ya chai bora duniani, ilikuwa na soko kubwa sana na zuri sana. Waliokuwa wanafuatilia mambo ya soko la chai wanajua jinsi gani ile chai ilivyokuwa na soko zuri duniani, lakini leo imepotea kwa sababu pengine ya ubovu wa njia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika Mpango wetu naomba tuangalie sana maeneo yale ambayo wakulima wanazalisha mazao mbalimbali hasa mazao ambayo yanaweza kuuzwa nchi za nje na yakatuingizia fedha za kigeni. Kwa hiyo, tukifanya hivyo, tutawawezesha wananchi hawa kwanza kuuza mazao yao, lakini pia hata bidhaa zetu ziwe na ubora na kwa kupitia hivyo tutaweza kupata fedha za kigeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia barabara zinapokuwa nzuri, tunawavutia wawekezaji. Tunasema tunaenda kwenye uchumi wa viwanda, wawekezaji hawawezi kwenda kuwekeza kwenye maeneo kama ya Lupembe ambapo barabara haipitiki wakati wa kifuku; maana yake ni kwamba, watapoteza kwa maana ya kwamba watazalisha lakini hizo bidhaa zao au mazao yao ambayo wamezalisha, hawataweza kuyauza yakiwa na ubora wake kwa sababu ya ubovu wa barabara. Kwa hiyo, maeneo haya ya uwekezaji ni lazima tuhakikishe kwamba barabara zinapitika muda wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, viwanda tunavyovifikiria, ni lazima viwekezwe au twende tukaviwekeze kwenye maeneo ambayo yana uzalishaji. Inakuwa haipendezi wala haina tija kwa mkulima kama kiwanda kinakuwa mbali na maeneo ambayo hawa wakulima wanazalisha. Inapokuwa hivyo ni kwamba, wananchi, wale wakulima wanakosa bei nzuri ya mazao kwa sababu hapo katikati wanacheza wale middlemen, wananunua bidhaa kwa wakulima kwa bei ya chini na wanawauzia wamiliki wa viwanda kwa bei ya juu. Kwa hiyo, tayari wakulima wetu wanapoteza soko la bidhaa zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili tuweze kuwahamasisha wakulima, lakini pia wakulima wetu waweze kupata tija ya mazao wanayozalisha, ni lazima tuwavutie hawa wawekezaji wa viwanda mbalimbali kwenye maeneo ambako hawa wakulima wanazalisha, ndipo hapo utaweza kuwasaidia wakulima wakapata tija kwa kilimo chao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda peke yake na barabara peke yake haitoshi. Ni lazima huduma za msingi hasa huduma za afya kwa maana ya Hospitali, Zahanati na Vituo vya Afya vijengwe kwenye maeneo haya ambayo kuna uzalishaji mkubwa, lakini pia kuna viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Njombe haina hospitali hata moja. Sasa hutegemei maeneo kama hayo wawekezaji watakuja kuwekeza kwa kuwa huduma ya afya haipo. Ni lazima tuangalie upande mwingine. Tunapotaka kuwekeza tuangalie na factors nyingine ambazo zinaweza zikasababisha wawekezaji waweze kuwekeza au inaweza ikasababisha viwanda vyetu viweze kukua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ilivyo sasa hivi ukiangalia hata kwenye Mpango, viwanda vingi vimeelekezwa mijini. Sasa vinavyoelekezwa mjini tunawanyima asilimia zaidi ya 80 ya wakulima wanaoishi vijijini au watu wa vijijini. Kwa hiyo, tukitaka kufungua fursa za ajira, ni lazima tufikirie sasa kuanza kuwekeza kwenye maeneo ambako wakulima wapo na vijana wengi wanaishi ili tufungue ajira huko vijijini, watu wabaki vijijini kuliko sasa hivi wote wanavyokimbilia mjini. Sasa kama watakimbilia mjini, nani atakayezalisha huko vijijini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema kwamba tunafungua viwanda kule Ludewa, sasa bidhaa nyingine ambazo zinategemea hivi viwanda, watapata wapi kama hatutaweka mazingira rafiki ya kuwawezesha vijana wetu waweze kubaki vijijini? Kwa hiyo, tunaomba kwenye Mpango pia tuweke vizuri ili hatimaye tuweze kuhakikisha kwamba tunaweza kufanikiwa hasa kuingia kwenye uchumi huu wa kati ambao ni uchumi wa viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nishati, nalo ni suala ambalo linaendana pamoja. Tukitaka tuvutie wawekezaji wa viwanda hivi vya kati na vikubwa, ni lazima tuhakikishe kwamba maeneo yetu mengi yanakuwa na nishati ya kutosha; yanakuwa na umeme wa kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ilivyo sasa hivi, kwa mfano, eneo langu ni la uwekezaji; kuna mazao mengi ambayo yana tija ambayo watu wengi wanaweza wakapata faida, lakini wawekezaji wanashidwa kuwekeza kwa sababu umeme siyo wa uhakika. Kwa hiyo, naomba Waziri wa Nishati pia katika Mpango huu tujaribu kulifikiria kuhakikisha kwamba tunasambaza umeme katika maeneo ya uzalishaji hasa maeneo ya Lupembe ambako kuna wawekezaji wengi wazuri, wanakuja lakini hawawezi kuwekeza kwa sababu hakuna nishati ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nijaribu kulisema kidogo juu ya Mpango huu, tujaribu kujadili juu ya kuhakikisha kwamba hawa vijana au wananchi ambao tumesema tutawezesha kwa kuwapa Shilingi milioni 50 kila Kijiji, ni lazima tutengeneze mpango mzuri hasa kwanza, kutoa elimu ya ujasiriamali; elimu ya matumizi ya hii mikopo ambayo tunaipanga iende kwa wananchi kule vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wengi walioko vijijini hawana elimu ya kutosha ya ujasiriamali, hawana uelewa wa kutosha wa ku-generate mkopo na mwisho wa siku wapate faida. Ni lazima tuweke mpango ni jinsi gani tutatoa elimu kwa wananchi wa vijijini ili mkopo huo wakiupata waweze kuutumia vizuri na mwisho wa siku waweze kupata faida na ile faida iweze kurudishwa na hatimaye tuweze kuongeza uchumi wa kila mmoja na hatimaye uchumi wa Taifa zima kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima tujipange kuhakikisha ni jinsi gani tutatoa elimu na siyo kutoa elimu tu; jinsi gani tutawasaidia katika kuwatafutia masoko ya bidhaa ambazo pengine watakuwa wanazalisha ili ule mkopo uweze kuleta tija? Tukiwaacha tu hivi hivi tukapeleka tu zile fedha, itakuwa kama ilivyokuwa yale mamilioni ya Kikwete. Zitaenda fedha nyingi na mwisho wa siku kitakachorudi, hakuna. Kwa hiyo, tutakuwa tumepoteza mamilioni mengi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo nafikiri inatosha. Nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa hotuba nzuri aliyoitoa leo tarehe 3 Mei, 2016. Pia, nampongeza kwa kujituma, kuwajibika vizuri katika kusimamia Wizara yake. Hii inaonesha kuwa Mheshimiwa Rais hakukosea kumteua katika Wizara hiyo. Ni matumaini yangu kuwa kupitia Waziri huyu, nchi yetu itapata mapinduzi makubwa ya kilimo, mifugo na uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo, napenda kutoa ushauri mdogo kwenye upande wa kilimo, hususan pembejeo. Serikali yetu ya Awamu ya Nne iliweka utaratibu wa kuwasaidia wakulima wetu kwa kuwapatia pembejeo za ruzuku.
Pembejeo hizi zimekuwa hazimsaidii mkulima hasa wakulima wadogo. Wafanyabiashara na makampuni yamekuwa yakiingia mikataba na Serikali ili kuwasambazia wakulima pembejeo hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Makampuni yamekuwa yakiwapatia pembejeo hizo kupitia mawakala kwa mtindo wa vocha. Mawakala hawa wamekuwa wakijinufaisha kwa kuwalaghai baadhi ya wakulima kwa kuwaomba wasaini vocha hizo bila kuchukua mbolea au pembejeo hizo kwa kuwalipa fedha kati ya sh. 5,000/= mpaka sh. 10,000/=.
Mheshimiwa Naibu Spika, mbolea hizi zimekuwa zikipelekwa kwa wakulima kiasi kidogo au kwa kuchelewa ili ziwakute wakulima wakiwa wamepanda na kuwashawishi wasaini vocha hizo. Kupitia tabia hizi za mawakala wasio waaminifu, Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuwasaidia wakulima kwa kulipia baadhi ya gharama za kilimo na pembejeo, lakini zimekuwa hazizai matunda. Naishauri Serikali ione au iweke utaratibu mwingine wa kuwasaidia wakulima kwa kulipia baadhi ya gharama za mbolea au pembejeo ili wakulima wawe huru kwenda kujinunulia mbolea hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, niliwahi kushuhudia wakala mmoja akielezea jinsi gani alivyonufaika na usambazaji wa mbolea hizo. Ni vizuri Serikali ifanye utafiti wa kutosha juu ya matumizi ya mbolea za chumvi chumvi kwa baadhi ya maeneo. Mbolea nyingi zinazoenda Mkoa wa Morogoro zimekuwa zikipelekwa Mkoa wa Njombe. Wakulima wengi wa Morogoro wamekuwa wakipelekewa mbolea hizo na kutochukua kwa kupewa fedha kidogo na badala yake mbolea hizi zimekuwa zikipelekwa Mkoa wa Njombe ambako mahitaji ni makubwa. Wafanyabiashara wamekuwa wakiuza mbolea hizo kwenye maduka ya kawaida na kupata faida kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiajiri vijana wengi wenye taaluma ya kilimo ili kuendelea kutoa mafunzo ya kilimo kwa wakulima wetu; Mafunzo ya matumizi mazuri ya mbolea, uchaguzi wa mbegu bora na mengineyo. Lengo ni kuongeza ujuzi wa kilimo bora kwa wakulima na kuongeza kiwango na ubora katika uzalishaji. Vijana hawa wamekuwa wakikaa tu maofisini bila kufanya kazi zao kama Maafisa wa Kilimo. Ni muhimu kwa Serikali kuweka utaratibu wa kuwafanya Maafisa hawa kuwajibika ipasavyo kwa maendeleo ya wakulima wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Maafisa Kilimo ni lazima pale wanapofanyia kazi wahakikishe kwamba, wanakuwa na kajishamba darasa (demonstration farms). Ili kuhakikisha kwamba kumekuwa na uwajibikaji wa Maafisa Kilimo, ni lazima kuwe na utaratibu wa kuweka malengo mahususi ya uzalishaji katika eneo husika na Maafisa hawa wapimwe kwa ufanisi wa malengo hayo. Kwa kuweka malengo hayo, Maafisa Kilimo wataweka utaratibu wa kushinda shambani na wakulima ili kuhakikisha kwamba malengo ya wakulima yanafikiwa na malengo yake Afisa yanafikiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, natoa shukrani zangu za dhati kwa kupata fursa hii ya kuchangia. Nawasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu, John Pombe Magufuli kwa kuanza kutekeleza Sera ya Elimu ya mwaka 2014, hasa kwa kuondoa au kwa kufanya elimu ya msingi na sekondari iwe elimu bure. Hii imewasaidia Watanzania wengi ambao walikuwa wanashindwa kupeleka watoto wao shule za msingi na sekondari kuweza kupata elimu. Kwa hiyo, imeongeza access to primary and secondary school education. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na changamoto ambazo Wabunge wameendelea kuzisema, lakini kwanza tumefungua access, tumewawezesha Watanzania wote waweze kupata fursa ya kupata elimu ya shule ya msingi na sekondari. Hizi changamoto nyingine tutaendelea kuzitatua kadri muda utakavyokuwa unaendelea. Kwa hiyo, lazima uanze kwanza kuweka fursa, lakini baadaye katika fursa unakuwa na changamoto nyingine nyingi ambazo tumesema kuna changamoto za miundombinu, changamoto za resources mbalimbali ambazo tutaendelea kuzifanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Waziri wa Elimu kwa kuteuliwa kuongoza Wizara hii, namwamini, yupo makini na atatufikisha pale ambapo tunatakiwa tufike, lakini pia nimpongeze Naibu wake wa Elimu, Mheshimiwa Stella Manyanya na nimpe pole kwa msiba aliopata wa mama yake. Mungu aendelee kumrehemu na aendelee kumpa nguvu katika kipindi hiki ili arudi kutekeleza majukumu muhimu sana ya elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika nianze kusema jambo moja linalowakera sana Walimu hasa madai ya Walimu. Pamoja na mambo mengine yote jambo la madai ya Walimu, ndiyo pengine yanachangia kuathiri kiasi kikubwa kufisha elimu au inachangia kwa kiasi kikubwa katika utoaji wa elimu. Walimu wanapokuwa wanadai nyongeza ya mishahara, wanapodai kupandishwa madaraja, hii inawakatisha tamaa. Kwa hiyo, muda mwingi wanakuwa wanawaza kuongezewa mishahara, muda mwingi wanawaza madai yao mbalimbali na changamoto mbalimbali, kwa hiyo, wanaenda kazini wakiwa wamevunjika moyo wa kufanya kazi, hivyo hawafanyi kazi vizuri. Pamoja na kwamba tumeajiri Walimu wengi lakini ukifika kwenye mashule tuna Walimu wengi sana, lakini wanaoingia darasani ni wachache, lakini katika wachache wanaofundisha ni wachache sana! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, walimu wengi wanaingia wakiwa wamekata tamaa, wanaingia wakiwa wanawaza maisha, wanawaza mishahara yao, anawaza atarudije nyumbani, anawaza ataishi namna gani kule nyumbani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe Wizara zinazohusika hasa, Wizara ya TAMISEMI, ihakikishe kwamba madaraja ya Walimu yanapanda kwa wakati na zile stahiki zao kwa maana ya madai yao ya likizo, madai yao ya mishahara mbalimbali na madai mengine yanatekelezwa kwa wakati ili Walimu wawe na moyo wa kufundusha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wote tunajua huwezi kuwa unafanya kazi vizuri zaidi, kama unakuwa na madai mbalimbali, kama unakuwa unalaumu vitu mbalimbali ambavyo hujatekelezewa. Kwa hiyo, niombe Wizara ya TAMISEMI wakishirikiana na Elimu pia, tuweze kuhakikisha kwamba, madai ya Walimu yanalipwa kwa wakati na pia madaraja ya Walimu yanapandishwa kwa wakati. Kuna huu upandishwaji wa madaraja baada ya miaka kadhaa, Walimu wengi wanaokwenda kusoma mara nyingi wamekuwa wakicheleweshewa sana kupanda madaraja yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wamekuwa wakirudi nyuma, akiondoka kwenda kusoma, akirudi anakuta Mwalimu aliyemwacha ambaye ana elimu ndogo kuliko yeye amepandishwa daraja na yeye anabakia nyuma. Kwa hiyo, hili nalo linakatisha sana tamaa Walimu. Kwa hiyo, niombe madaraja ya Walimu yaende sambamba na muda aliyofanya kazi lakini sambamba pia na elimu yake aliyoipata ili angalau tuweze kuwamotisha hao Walimu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niseme jambo moja lingine ambalo wamesema Waheshimiwa Wabunge wengi sana juu ya mikopo ya elimu ya juu. Hili nalo limekuwa ni tatizo kubwa wale walengwa ambao wanatakiwa kupewa mikopo wamekuwa hawapati, hasa watoto wa maskini wanaoishi huko Vijijini, wanapewa wakati mwingine asilimia ndogo, asilimia 40 au wakati mwingine asilimia 30 na mwisho wa siku wanashindwa kulipa ada wanabaki wakihangaika tu na wengine imefika mpaka wakati mabinti zetu wanaanza kutafuta njia nyingine za kuweza kupata fedha za kujikimu wanapokuwa chuoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tuombe uwekwe utaratibu mzuri kama tulivyosema kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, wanafunzi wote watakaokuwa wamedahiliwa kwenda chuo kikuu kwa kuwa wana sifa ya kusoma chuo kikuu wapewe mikopo asilimia 100 na kwa sababu ni mkopo wapewe wote kuliko kuweka haya madaraja kwa maana wengine wanapewa asilimia 80, wengine 70, wengine 60 na 40; hiyo inaleta matatizo na inaleta migomo na maandamano yasiyo na tija. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuombe Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Elimu alisimamie hili, wanafunzi wote wanaokuwa wamedahiliwa kwenda chuo kikuu, basi wapewe mikopo asilimia 100 ili tupunguze baadhi ya matatizo ambayo wamekuwa wakipata hawa wanafunzi wa vyuo vikuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema na Wabunge wengi wamesema juu ya changamoto za Walimu wa sayansi kwamba Walimu wa sayansi hawapo au wapo wachache, kwa mfano kwenye Jimbo langu la Lupembe Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, tuna upungufu wa Walimu wa sayansi 93 na wakati huo huo tuna upungufu wa Walimu 158 wa shule za msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunasema kwamba, tunataka twende kwenye uchumi wa kati, uchumi wa viwanda, hatuwezi kwenda kwenye uchumi huo kama hatutakuwa na Walimu wa sayansi wa kutosha. Kwa hiyo, naomba kwanza kabisa tuanze kuwahamasisha wanafunzi wetu toka shule za misingi waweze kupenda masomo ya sayansi. Walimu wa shule ya msingi wawa-encourage watoto waweze kupenda hisabati, waweze kupenda masomo ya sayansi na hatimaye wakifika sekondari waanze kupenda kusoma masomo ya sayansi, ni uamuzi tu, tuwaweze hawa Walimu wanaofundisha, tuwawezeshe Wakuu wa Shule pia ili waweze kusimamia vizuri kuhakikisha kwamba katika shule zao wanafunzi wanafaulu masomo ya sayansi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ku-declare interest nami ni Mwalimu, nimekuwa Mkuu wa Shule, shuleni kwangu wanafunzi hakuna option, wanasoma masomo yote yale ya msingi, yote yale tisa na wanafaulu zaidi sayansi hata kuliko art. Kwa hiyo, tukiamua tukaweka miundombinu vizuri, tukaweka mazingira mazuri, wanafunzi wanaweza wakafaulu vizuri masomo ya sayansi na hatimaye tukapata wanafunzi wanaokwenda vyuo vikuu kusomea masomo ya sayansi, kwa hiyo, tutaweza kutokomeza jambo hilo, tutaweza kusaidia kupunguza uhaba wa Walimu wa kuanzisha utaratibu wa kuweza kuwahamasisha watoto wa shule za sekondari waweze kupenda masomo ya sayansi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo moja kama nilivyosema, la nyumba za Walimu, katika shule zetu nyingi hasa za Kata tuna uhaba mkubwa sana wa nyumba za Walimu, hata katika Jimbo langu tuna uhaba mkubwa sana wa nyumba za Walimu. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Elimu na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI watakavyopanga katika ujenzi wa zile nyumba zile 30 ambazo zinachukua Walimu wengi na mimi wanifikirie kule kwangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna shule mbili hazina hata nyumba za Walimu kabisa, shule ya Ndinga na shule ya Mrunga kule, kwa hiyo, mnisaidie ili niweze kupata hizi nyumba angalau na Walimu wangu waweze kukaa katika maeneo ya shule na hivyo kufundisha zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna jambo linguine, wamesema la Mdhibiti wa Ubora, zamani tulikuwa tunaita Kitengo cha Ukaguzi, lakini niseme kwamba Mkaguzi wa kwanza ni mkuu wa shule, tumwezeshe mkuu wa shule aweze kusimamia shule yake vizuri na hatimaye tuwezeshe Kitengo cha Udhibiti Ubora cha Halmashauri au cha Wilaya ili waweze kuhakikisha kwamba wanafanya kazi zao vizuri na Wakaguzi wa Kanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi wakaguzi hawana fedha kabisa, hawana fedha za mafuta, wanashindwa kwenda kwenye mashule kwenda kukagua. Sasa huwezi kuamini kwamba kama Mkaguzi hawezi kufika kwenye shule kwenda kufannya ukaguzi, je, huko shuleni kutakuwa na kitu gani? Atajuaje ubora kama upo kwenye shule hizo husika. Kwa hiyo, tuombe Wizara husika nazo ziwawezeshe hawa Wadhibiti Ubora kwa maana ya Wakaguzi wetu wa Halmashauri, Wakaguzi wetu wa Knda, lakini pia tumwezeshe Mkuu wa Shule aweze kusimamia vizuri taaluma kwenye shule yake kwa kuwa yeye ni mkaguzi wa kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, iliwekwa ile pesa ya majukumu, sh. 200,000/= kwa Walimu wakuu; Sh. 250,000/= kwa Wakuu wa Shule na sh. 300, 000 kwa Wakuu wa Vyuo. Tukiwapa hizi fedha wataweza kusimamia taaluma vizuri, wataweza kukagua vizuri na kuhakikisha kwamba Walimu wao wanafundisha vizuri. Ilivyo sasa hivi unaweza ukafika Mkaguzi wa Halmashauri au wa Kanda akafikiri Mwalimu anafundisha vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, wanachofanya darasani kule wanatoa notes, wanatoa kazi, wanasahihishana mle darasani, halafu mwisho wa siku akija Mkaguzi, anaangalia madaftari anakuta kuna mazoezi ya kutosha, anaangalia lesson plan na schemes of work zimekaa vizuri, lakini kumbe kinachoendelea darasani sicho hicho kilichopo kwenye hivi vitabu mbalimbali. Kwa hiyo, tuwawezeshe kwanza Wakuu wa Shule ambao wako jirani na baadaye Idara nzima ya Ukaguzi ili tuweze kuboresha elimu.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kidogo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kupongeza Baraza zima la Mawaziri na Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa wanayoifanya hasa kuhakikisha kwamba Tanzania inakuwa ni Tanzania ya Viwanda. Nawapongeza sana! Kwa namna ya pekee nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kazi kubwa anayoifanya hasa kuhakikisha kwamba tunafikia azma ya kuwa na viwanda au kufikia uchumi wa viwanda katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema kwamba hatuwezi kufikia huo uchumi wa viwanda bila kufikiria Sekta ya Kilimo. Sekta ya Kilimo ndiyo sekta mama ambayo itatuwezesha sisi Watanzania kuingia kwenye uchumi wa viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua sote kwamba zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania ni wakulima, sasa huwezi kuiacha sekta hiyo ya kilimo ukaingia kuwekeza viwanda vya aina nyingine na ukataka kufika kwenye uchumi wa viwanda. Kwa hiyo, ni lazima tuitazame Sekta ya Kilimo, tufikirie kuwekeza kwenye viwanda vya kilimo. Historia inatuambia kabisa kwamba hata nchi zilizoendelea, tunafahamu wote nchi za Uingereza, Ujerumani na Marekani walianza kwanza na viwanda vya Sekta ya Kilimo; Agro Processing Industries ambavyo vilikuwa vinaongeza value ya mazao au thamani ya mazao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nasi Watanzania tukitaka twende huko kwenye uchumi wa viwanda ni lazima tuangalie wakulima wetu waweze kuwa na viwanda ambavyo vitaongeza thamani ya mazao yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukishakamilisha kuwa na viwanda vya uongezaji wa thamani ndipo hapo sasa hawa wakulima watahitaji zana mbalimbali, watahitaji magari ya kusafirishia, basi itafanya sasa kuwe na demand ya vitu vingine ambavyo hivyo sasa vitahitaji viwanda vya mechanical industries na baadaye tutaingia pengine kwenye Chemical Industries.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nami nasema kwamba, ni muhimu Waziri wetu wa Viwanda aanze sasa kuangalia maeneo hasa ya uzalishaji ili kuwavutia Wawekezaji ili waweze kuwekeza viwanda vya kuongeza thamani kwenye mazao yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiweza kuongeza thamani ya mazao, kwanza kabisa itatusaidia kutoa ajira kwa vijana wetu. Tunatambua vijana wengi wako huko vijijini na sasa hivi wanakimbilia mijini wakifikiria kutafuta kazi kwenye Maofisi au kwenye viwanda mbalimbali na wakifika huko wanakosa hizo ajira. Sasa tuanze kufikiria kuanzisha viwanda hivi vijijini ili vijana wetu wengi waweze kuajiriwa kwenye viwanda hivyo, wabaki kule na kufanya kazi ya uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapata changamoto moja kubwa; mimi natokea Jimbo la Lupembe ambapo tunazalisha chai, kahawa, tunazalisha mazao ya matunda, kama mananasi, ndizi, machungwa na matunda mengine mengi tu, lakini kule Lupembe mpaka sasa hivi wale wananchi hawawezi kuuza mazao yao vizuri kwa sababu ya tatizo moja na hata Wawekezaji hawapendi kuwekeza maeneo yale kwa sababu ya tatizo la miundombinu.
Mheshimiwa Naibu Spika,kwa hiyo, lazima tunapofikiria uchumi wa kati, tunapofikiria uanzishwaji wa viwanda kama nilivyosema lazima tuhakikishe kwamba kwenye maeneo ya uzalishaji ambapo huko ndiko tunategemea kuanzisha viwanda, ni lazima miundombinu ya barabara, tuhakikishe kwamba tunakuwa na barabara nzuri ambazo zinapitika muda wote ili watakaowekeza waweze kusafirisha hizo bidhaa kirahisi zaidi na hatimaye kufikia soko au kufikia maeneo ambayo wanaweza wakaongeza thamani zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia lazima tufikirie kuwekeza kwenye umeme. Kwa hiyo, unaona hapo Wizara nyingi sana zinahusika. Ni lazima tuwe na umeme wa kutosha kwenye maeneo haya ili tuweze kuwavutia wawekezaji waweze kuwekeza kwenye maeneo haya ya uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, ni lazima tuwe na maji. Tukiwa na maji ya kutosha automatically tutavutia wawekezaji, kwa sababu naamini kwamba, siyo Serikali itakayokwenda kujenga viwanda, wanaojenga viwanda ni wawekezaji wa ndani na nje. Sasa hawa lazima kuwe kuna huduma hizi muhimu. Huduma za maji, umeme, lakini pia huduma za afya ni lazima ziwe za kutosha ili wawekezaji waweze kuwekeza kwenye maeneo ya vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ilivyo sasa kwenye maeneo mengi ya uzalishaji, watu hawapendi kwenda kuwekeza kwa sababu hizi huduma muhimu hazipo. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri, tunapotaka kuwekeza, ni lazima tufikirie mambo hayo muhimu na hasa tufikirie kuwekeza kwenye kilimo ambacho kwanza viwanda vyenyewe ni vya bei ndogo, ni rahisi kuwekeza, lakini pia vinaweza vikaajiri Watanzania wengi na katika sera yetu tumesema kwamba lazima tuanzishe viwanda, tuanzishe shughuli ambazo zitawaajiri vijana wengi kwenye sekta mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ili tuweze kupata uwekezaji mzuri na hatimaye uwekezaji ukawa na tija, ni lazima tufikirie maeneo ya kuwekeza, hasa maeneo yale ambayo kuna uzalishaji, maana tunaweza tukawekeza kama ilivyokuwa kwenye viwanda vile vya tumbaku, badala ya kuwekeza Songea na Tabora ambako tumbaku inazalishwa, vikawekezwa Morogoro. Hatimaye utakuta wakulima wanakata tamaa kwa sababu hawawezi kusafirisha mazao yao kuyaleta Morogoro. Kumbe viwanda hivi vingekuwa vimewekezwa sehemu zile ambazo wanazalisha, basi wakulima wangeweza kupata faida kubwa na wangehamasika kuzalisha hilo zao na hatimaye nchi kupata faida kubwa au uchumi wetu kuweza kukua kwa kuwa viwanda vimewekwa kwenye maeneo ya uzalishaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunapoweka viwanda kwenye maeneo ya uzalishaji tunawasaidia wakulima wetu kuweza kupata faida katika kilimo. Ilivyo sasa hivi wanaofaidika sio wakulima, wanaofaidika ni wale middlemen, wale watu wanaonunua mazao toka kwa wakulima na kwenda kuwauzia watu watu wenye viwanda.
Kwa hiyo, haiwasaidii wakulima kama tutawekeza viwanda vyetu mbali na kule wanakozalisha. Kwa hiyo, tuweke jirani na eneo la uzalishaji ili wakulima wetu waweze kuuza mazao yao na kupata faida na hatimaye Taifa lipate faida kupitia viwanda na ajira hizi ambazo tumewekeza kupitia viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nijaribu kuongelea suala la kodi. Mara nyingi kumekuwa na kodi nyingi sana kwenye mazao, hasa mazao ya biashara. Kwenye zao la chai, kahawa, tumbaku na pamba, kuna kodi nyingi au kuna utitiri wa kodi. Utakuta kodi za mazao haya hufika mpaka 20 nyingine mpaka 25 au 27. Sasa mwisho wa siku anayekuja kulipa hizi kodi zote ni mkulima. Kwa hiyo, utakuta kupitia hizi kodi, tunamnyonya huyu mkulima ambaye kwanza anapata shida sana kuzalisha hili zao na soko lake halina uhakika; sehemu ya kuuzia kwenye kiwanda, hakina uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho wa siku anauza zao lake; anauza chai yake, kahawa, pamba au tumbaku yake kwa bei ya chini kwa sababu ya kuwa na kodi nyingi. Kwa hiyo, tunapofikiria viwanda au uzalishaji ni lazima tufikirie pia na hizi kodi, tujaribu kuzipunguza ili angalau mkulima aweze kupata faida. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kuhusu wawekezaji wazawa. Mara nyingi tumekuwa tukiwavutia wawekezaji wa nje tunawasahau wazawa. Tunasahau kuwahamasisha wananchi wale wanaotaka kujiunga kwenye vikundi vidogo vidogo na kuanzisha viwanda au kuna maeneo mengine tayari kuna wakulima ambao wameonesha nia ya kuwekeza kwenye kilimo na kwenye viwanda, ni vizuri Serikali tuwe na utaratibu wa kuhakikisha kwamba tunawawezesha kwa kuwapa mikopo au kwa kuwasaidia kuweza kupata mikopo rahisi na kuweza kuwekeza kwenye viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwangu kuna mkulima mmoja anataka kuwekeza kwenye kiwanda cha chai, kwenye processing industries, lakini anashindwa kupata utaratibu gani mzuri ili aweze kupata mkopo na hatimaye aweze kufungua kiwanda cha chai. Kwa hiyo, naomba tunapofikiria uwekezaji, tuwafikirie sana Watanzania wenzetu ambao wanataka kuwekeza kwenye viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Waziri wangu wa viwanda ajaribu kuhamasisha au kututafutia wawekezaji wengi kwenye mazao ya chai. Kule Lupembe tuna viwanda viwili tu na vile viwanda haviwezi kutosha, havikidhi mahitaji ya chai ya Lupembe. Lupembe tunazalisha chai nyingi na vile viwanda viwili haviwezi ku-process ile chai yote, matokeo yake chai nyingi zinamwagwa na wananchi wanapata hasara kubwa sana. Kwa hiyo, naomba, kama kutakuwa na mwekezaji wa kiwanda cha chai, tunaomba aje awekeze Lupembe.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye matunda, nanasi na…
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kidogo kwenye Wizara hii ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kuwapongeza Mawaziri; nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu kwa kazi kubwa anayofanya, anavyojituma kufanya kazi kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata hii huduma ya afya vizuri kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Naibu Waziri wake, naye ni jembe, anafanya kazi vizuri sana, tunaomba mwendelee hivyo hivyo, katika kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma ya afya hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia yangu machache niseme kidogo juu ya huduma ya afya hasa kwenye maeneo ya vijijini. Nafikiri wote tunatambua kwamba Watanzania wengi wanaishi vijijini na ndiko huko Watanzania hawa wanapata matatizo makubwa sana ya huduma za afya. Kwa hiyo, tunapotaka kuboresha ni lazima tuwafikie hasa Watanzania walio wengi wanaoishi maeneo ya vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sera yetu imekaa vizuri kwamba kila kwenye kijiji tuwe na Zzhanati na kila kwenye Kkta lazima pawe na kituo cha afya na angalau kwenye Halmashauri kuwe na huduma ya hospitali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niende kwenye Jimbo langu. Jimbo langu lina vijiji 45, lakini zaidi ya asilimia 70 kuna zahanati. Tukija kwenye vituo vya afya, tuna viwili tu. Kimoja kipo Lupembe, kilometa takriban 80 kutoka Njombe Mjini au toka kwenye Hospitali ya Wilaya ambayo ipo Halmashauri ya Mji na kingine kipo maeneo ya Kichiwa karibu kilometa 50 toka mjini. Kwa hiyo, unaweza ukaona jinsi gani wananchi wa maeneo haya wanavyopata shida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa kwangu kule, kuna baadhi ya watu wanatembea zaidi ya kilomita 47 ili kupata huduma ya zahanati. Mgonjwa anatembea kilomita saba ili aweze kupata angalau huduma ya zahanati. Akikosa hapo anatembea umbali mwingine zaidi ya kilomita 25; angalau kukutana na kituo cha afya, halafu akitoka hapo akishindwa kupata huduma, anatakiwa kutembea takriban umbali wa kilomita 80 kwenda kwenye Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema kwamba kwenye Jimbo langu hakuna Hospitali ya Wilaya wala ya Serikali hata tu zile za binafsi, hazipo. Kwa hiyo, tuombe Wizara katika mipango yenu ya uboreshaji, angalau muwafikirie wananchi hao walio wengi wanaoishi vijijini. Hasa sehemu kubwa wanaoathirika hapa ni akinamama na akinamama wajawazito. Kule kwangu kwa sababu ya ubovu wa njia, hospitali kuwa mbali na vituo vya afya kuwa mbali, wengi wao wamekuwa wakijifungulia njiani, wakipoteza maisha wakiwa njiani kwenda kwenye Hospitali ya Wilaya kwa ajili ya kupata huduma ya upasuaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba katika mipango ya Wizara pia kwa kushirikiana na Wizara ya TAMISEMI angalau tuhakikishe kwamba vituo vya afya vilivyoko vijijini, viwe na huduma ya upasuaji ili tuweze kuokoa maisha ya akinamama wengi wa Tanzania wanaopoteza maisha yao wakati wanapotimiza haki yao ya msingi ya kuongeza watu hapa duniani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kama walivyosema wenzangu juu ya huduma ya CHF (Community Health Fund), inawasaidia wananchi wengi hasa wa vijijini na wengi wao wanaifurahia huduma hii. Lipo tatizo moja, kwamba wakishakatiwa hii CHF, haitumiki kwenye kata nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri ziweze kuunganishwa na Hospitali za Wilaya. Wakishakatiwa hii CHF basi waweze kuitumia hata kwenye Hospitali ya Wilaya au kwenye hospitali iliyo katika kata nyingine, ili kama anakosa matibabu, huduma au dawa hazipo kwenye hospitali ya Serikali au kwenye Kituo cha Afya cha Serikali, basi aweze angalau kwenda kwenye Hospitali ya Wilaya na akapata matibabu; kuliko ilivyo sasa hivi, wagonjwa hawa au wananchi wetu wakikosa kwenye kituo cha afya pale hawezi kwenda sehemu nyingine akatumia CHF. Kwa kuwa tumesema kwamba sasa matibabu yatakuwa yanatumika pia na TEHAMA, kwa kuwa jina litakuwa lipo kwenye database basi aweze kutibiwa sehemu nyingine kwa kutumia hii huduma ya CHF.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo juu ya matibabu kwa wazee kama walivyoongelea wenzangu. Wazee wetu wanapata shida na tumesema kwenye ilani kwamba sasa tutaboresha huduma hasa kuhakikisha kwamba wazee wetu walio na umri unaozidi miaka 60 waweze kutibiwa bure. Bado kuna changamoto kubwa, kwa kuwa hospitali nyingi au zahanati na vituo vya afya vingi havina dawa za kutosha, hawa wazee wetu wamekuwa wakikosa matibabu. Tukumbuke kwamba wazee wetu hawa hawana uwezo wa kuzalisha, kwa hiyo, hawana uchumi mzuri, hawana fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri kwamba ni vizuri sasa badala ya kuwapa CHF, wapewe Bima ya Afya. Kwa kuwa ni wachache, basi Serikali ione umuhimu ya kuwapangia bajeti maalum wazee wote waliofikisha miaka 60 na wakapewa Bima ya Afya ili waweze kwenda kutibiwa kwenye hospitali zozote zilizoko hapa nchini kama ilivyo kwa wanufaika wengine wa Bima za Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo lingine juu ya miundombinu. Hospitali zetu na vituo vya afya vingi miundombinu yake bado siyo mizuri kwa maana ya huduma kama vile za umeme na maji. Utakwenda hospitali nyingi, utakuta zimejengwa vizuri, au kituo kimejengwa vizuri lakini hakuna maji. Naomba katika sera, katika mpango kwamba kila panapojengwa kituo cha afya au hospitali na maji pia yaweze kupelekwa katika maeneo hayo ili kuwepo na huduma bora. Wagonjwa wanaokwenda kwenye vituo hivi vya afya au hospitali basi wapate na huduma ya maji safi, kuliko ilivyo hivi sasa ambapo utakuta kuna hospitali nzuri, lakini inapofika kwenye huduma ya maji, haipo. Kwa hiyo, wanachota sehemu nyingine mtoni. Sasa hii ni hatari kwa mgonjwa kama kutakuwa na hospitali ambayo haina maji ya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni umeme. Tumeona kwenye hospitali nyingi sana hasa zilizoko vijijini, hazina hata umeme! Tupeleke umeme! Kama siyo kupeleka umeme ule wa REA basi tuwe na mipango ya kupeleka umeme wa solar, unaweza ukasaidia. Kwa hiyo, kila tunapojenga hospitali au tunapopeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ni lazima tufikirie pia na umeme, tuanze kufikiria na power itakayotumika kwenye kijiji, kituo cha afya au hospitali, ili wananchi waweze kupata umeme kwenye hizi hospitali zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho niseme kama walivyosema wenzangu juu ya unyanyasaji wa kijinsia. Tunaomba tuweke mipango rasmi kabisa ya kuhakikisha kwamba unyanyasaji wa kijinsia nchini kwetu unatokomezwa. Mpaka sasa hivi kuna maeneo mengine, akinamama ambao wamefiwa na waume zao, wanalazimishwa kwenda kuolewa na wadogo wa wenzi wao waliofariki. Bado kuna maeneo mengine wanalazimishwa kugawanya mali. Maana ndugu wanachukua mali za huyu marehemu aliyefariki, eti kwa sababu ya kulelea familia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tujaribu kujitahidi kuhakikisha kwamba akinamama wanaopoteza wenzi wao wajane hawa, wanatetewa na mali zao zinabaki kwa ajili ya kuendelea kuhudumia familia zao kuliko ilivyo sasa hivi kwa baadhi ya maeneo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Elimu. Kwanza nianze kwa kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa uamuzi wake mzuri kabisa wa kuamua kujenga mabweni ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mabweni haya yamejengwa kwa shilingi bilioni 10 na yataweza kutosha kuwa-accommodate wanafunzi 3,840. Nimpongeze sana kwa jitihada hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, nimpongeze Waziri wa Elimu na Naibu wake na pia Katibu wa Wizara na watendaji wote wa Wizara ya Elimu kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya katika kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata elimu na kupitia elimu hiyo tuweze kupata maendeleo katika nchi yetu maana bila elimu hakuna maendeleo. Kwa hiyo, nawapongeza sana kwa kazi kubwa ambayo mnaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu kama walivyosema wenzangu ni msingi wa kila kitu. Elimu ndiyo msingi wa maisha, bila elimu hakuna maisha. Kwa hiyo, ili tuweze kupata elimu nzuri ni lazima kuwepo na mwalimu, miundombinu mizuri lakini pia ni lazima tuwe na vitabu vya kufundishia na kujifunzia. Mimi nizungumzie juu ya walimu, walimu tunao japo tuna upungufu lakini kuna changamoto nyingi ambazo wanakabiliana nazo na ndiyo maana unakuta sasa inapofika katika kupata ile outcome tunakuwa na matatizo kwa sababu hatujawaweka vizuri walimu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamesema Waheshimiwa Wabunge hapa juu ya madeni ya walimu. Haya madeni ndiyo kikwazo katika utoaji wa elimu bora. Kwa wale waliowahi kuwa darasani (walimu) wanajua, mwalimu ili aweze kufundisha vizuri ni lazima awe vizuri psychologically. Huwezi kutegemea mwalimu akafundisha vizuri na akawawezesha watoto kupata elimu nzuri kama psychologically yupo disturbed. Mwalimu anapokuwa na madeni, mwalimu anapokuwa na kero mbalimbali za kwake binafsi ni vigumu kufundisha vizuri. Anaweza akaingia darasani akajipanga kutaka kufundisha vizuri wanafunzi lakini akikumbuka tu deni wakati anaendelea na jukumu la kufundisha, tayari huyu mwalimu hataweza kufundisha vizuri wanafunzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuipongeze Serikali mmeanza kulipa lakini bado speed ya ulipaji wa haya madeni sio nzuri sana. Tumeambiwa hapa na Kamati imetoa taarifa kwamba madeni ya walimu ambayo wanaidai Serikali mpaka sasa ni shilingi trilioni 1.6 na madeni yaliyolipwa ni shilingi bilioni 33.1 ambayo ni sawa tu na 32%, speed hii bado ni ndogo. Tuiombe Serikali iweze kulipa madeni haya. Tunajua madeni yanazidi kuongezeka kwa sababu wanapopandishwa madaraja madeni yanaongezeka na kwa kuwa yanaongezeka ni vizuri yalipwe mapema haya mengine ambayo yapo ili kupunguza sasa walimu wengi ambao wanakuwa frustrated. (Makofi)

Mheshimia Mwenyekiti, hali iliyopo sasa hivi na ukizingatia kuna mambo haya ya vyeti fake na ukaguzi na walimu wengine wameambiwa kuna baadhi ya vyeti havipo halali na hawajajua hatma yao. Kwa hiyo, hali iliyopo sasa hivi kwenye mashule walimu wengi hawafundishi bali wanahudhuria madarasani wanaofundisha ni wachache. Wengi wao wamekuwa disturbed na haya madeni na vyeti fake. Kwa hiyo, naomba Serikali yangu Tukufu tujaribu kujipanga kulipa madeni haraka lakini pia na hili zoezi la vyeti fake hili liweze kukamilishwa haraka ili walimu waingie darasani wafundishe wasiingie darasani kuhudhuria tu vipindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali na Waziri nafikiri anaelewa vizuri naposema mambo haya. Nafikiri atayashughulikia vizuri ili walimu wetu waweze kuendelea kufundisha na hatimaye tuje kuweza kutoa elimu bora. Tusipofanya hivyo, tutaendelea kuwaweka wanafunzi shuleni wanashinda wanacheza, wanakula chakula, wazazi wanafikiri watoto wanasoma kumbe hawasomi. Hata walimu wakuu wanafikiri walimu wanaingia darasani kumbe humo darasani hawafundishwi, mwisho wa siku matokeo yake yatakuwa ni mabaya. Kwa hiyo, niombe tukamilishe hili zoezi la vyeti fake lakini pia tukamilishe kulipa madai ya walimu ili walimu wetu hawa waweze kufundisha vizuri darasani na watoto wetu waweze kupata elimu nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine upande wa walimu pia, kuna upungufu mkubwa sana wa walimu katika shule zetu za msingi ukilinganisha na sekondari. Shule nyingi hazina walimu wa kutosha, vivyohivyo na hii inaathiri matokeo, inaathiri mwisho wa elimu kwa ujumla. Kwa hiyo, tuombe mamlaka zinazohusika ziajiri walimu. Tumeshaona kwenye hili zoezi la vyeti fake nalo limeondoa walimu wengi sana hasa wa shule za msingi. Ukiangalia idadi kubwa ya walimu wenye matatizo ya vyeti fake ni wale walimu wanaofundisha shule za msingi, kwa maana hiyo tufanye replacement haraka ili ku-rescue situation inayoendelea kwenye hizo shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna upungufu mkubwa sana wa walimu wa elimu maalum kwenye shule zetu hasa shule zetu za msingi. Kwa mfano, kwenye Halmashauri yangu mimi tuna shule moja pale ya Matembwe ambayo yenyewe ni shule jumuishi, inachukua wanafunzi ambao wana ulemavu tofauti tofauti, lakini tuna mwalimu mmoja tu anayefundisha kwenye ile shule. Kwa hiyo, tuombe tupeleke walimu wa kutosha na pia vifaa vya kutosha kwenye elimu hii jumuishi ili watoto hawa ambao wana ulemavu tofauti tofauti waweze kupata haki yao ya msingi, haki yao ya kupata elimu kama watoto wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema juu ya drop outs hasa hizi kesi za mimba kwenye shule zetu. Ukiangalia shule nyingi ambazo watoto wanapata mimba ni zile shule za kutwa, shule hizi za kata. Kwa nini wanapata mimba? Ni kwa sababu ya ukosefu wa mabweni. Watoto wengi wa kike wanatembea umbali mrefu sana na tunajua watoto wetu wa siku hizi hawawezi kutembea kama tulivyokuwa tunatembea sisi zamani. Kwa hiyo, kinachotokea ni kwamba wanatumia usafiri wa bodaboda maeneo mengine wanatumia taxi. Hawa wanaowapeleka shuleni ili waweze kuwahi vipindi ndio hao wakati mwingine wanawageuka kuwashawishi watoto kuingia kwenye hivyo vitendo vya ngono na mwisho wa siku wanapata mimba na wengine wanapata maambukizi ya UKIMWI na wengine wanaamua kuacha shule kwa sababu tayari wameshapata wapenzi na wanaenda kuolewa. Tunaipongeza Serikali kwa mpango huu wa kujenga mabweni.

Naomba pia katika Jimbo langu na katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Njombe na shule za kata za kutwa ambazo watoto wengi wanatembea umbali mrefu, katika ule mpango wa ujenzi wa mabweni basi na mimi nipate mabweni ili tuwaokoe watoto hawa ambao wanatembea umbali mrefu tuwakinge na mimba ambazo wanaweza wakazipata kutokana na vishawishi wanavyovipata njiani wanapoenda kwenye shule hizi za sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia umbali unachangia wanafunzi wetu kufeli. Wanatumia muda mwingi kutembea kwenda shuleni, anapomaliza kipindi anafikiria kuanza kutembea kwenda nyumbani na akifika nyumbani anakutana na shughuli za nyumbani kwa sababu ni watoto wa kike wanapewa shughuli za pale nyumbani za kupika, kutafuta maji, za kutafuta kuni lakini mwisho wa siku utakuta huyu mtoto anapoteza muda mwingi wa kusoma. Kumbe akibaki bwenini anapata muda mwingi wa kusoma na kufanya discussion na wenzake jioni mwisho wa siku atakuja kufaulu vizuri. Kwa hiyo, nashauri tujenge mabweni kwenye shule zote hizi za sekondari ili watoto wetu waweze kusoma vizuri na hatimaye waweze kupata elimu bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikitishwa sana kwenye suala la vitabu. Kwanza niipongeze Serikali kwa kuamua kutoa kitabu kimoja nchi nzima cha kufundishia (text book). Nipongeze kwa jitihada mlizochukua, lakini nisikitike kwa kutoa vitabu ambavyo vina makosa, ni aibu kubwa sana wakati tuna wataalam wameajiriwa, wanafanya editing ya hivi vitabu, inakuwaje vitabu vingi namna hii vinakuwa na makosa mengi ya spelling, ya kisarufi na makosa mengine? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe ndugu yangu, dada yangu Mheshimiwa Profesa Ndalichako, tukae na watu wa editing ili tujue nini kimetoea? Maana tumetumia fedha nyingi na itatakiwa tubadilishe tutatumia gharama kubwa, watuambie ni kwa nini wamekubali kutoa vitabu hivi ambavyo vina makosa? Haijawahi kutokea katika miaka yangu yote ya kusoma kwangu na katika maisha yangu yote kupata mwaka ambao vitabu vimetoka na makosa mengi namna hii, zaidi ya vitabu vya masomo karibia matano, sita, vina makosa!

Kwa hiyo, hebu tukae tujue kuna nini kimetokea? Inawezekana hao watu wanaohusika na editing walitaka kuhujumu tu Serikali ili kuonesha kwamba Serikali yetu haifanyi kazi vizuri. Nakuamini dada yangu, naomba kakae na hii Kamati au Kitengo kinachohusika na mambo ya editing ya vitabu ili tujue ni kwa nini wametoa vitabu vyenye makosa namna hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana kwa kunipa nafasi hii. Nami nianze kwanza kabisa kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwatumbua wote wabadhirifu na mabaradhuli wote wanaoharibu uchumi wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa namna ya pekee niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri wote na Manaibu Waziri kwa kazi kubwa wanazofanya hasa za kuhakikisha kwamba uchumi wan chi hii unakua. Lakini nimpongeze pia Waziri wa Nishati na Madini, Mheshimiwa Profesa Muhongo na Naibu wake Waziri kwa kazi kubwa wanayofanya kwa kuhakikisha kwamba Tanzania inakuwa na umeme wa kutosha na hatimaye tuweze kuwa na viwanda vya kutosha na shughuli nyingine za uchumi ziweze kuboreshwa kupitia umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee nimpongeze tena Mheshimiwa Waziri, nirudie, kwa kuhakikisha kwamba Jimbo langu la Lupembe pia linapata umeme. Nashukuru katika wiki hii vijiji viwili vimeweza navyo kupata mwanga wa umeme kwa mara ya kwanza kati ya vijiji 45; kwa hiyo, bado vijiji 33 havina umeme kati ya vijiji 45. Niombe Mheshimiwa Waziri na vile vijiji 33 vilivyobakia tuendelee kuvipigania ili viwe na umeme nao wajisikie wapo nchini Tanzania kama Watanzania wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kwamba maendeleo ni umeme. Uwepo wa umeme kwa maana ya nishati ya kutosha ya umeme na nishati yenye uhakika, lakini pia yenye bei nafuu ndipo tutaweza kuwa na maendeleo, lakini kama nishati itakuwa bado bei yake ipo juu wananchi wengi hawawezi ku-afford kuipata bado hatutaweza kuhakikisha kwamba tunaenda kwenye uchumi ambao tunauhitaji.
Niseme kwanza nipongeze kwa kupunguza bei, na umeme toka 1.5% mpaka 2.4%, lakini pia nipongeze kwa kutoa tozo la maombi ya uunganishaji wa umeme ambayo ni application fee shilingi 5,000; lakini pia nipongeze kwa kutoa service charge, hii ilikuwa inawakwaza wananchi wengi sana. Na nipongeze kwa niaba ya wananchi wangu wa Lupembe kwa kupunguza hii kodi maana wananchi kipato cha chini, wataweza kuingiza umeme kwa kutumia tu angalau shilingi 5,000 wanaweza wakapata umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuzungumzia kuhusu mradi wa REA. Katika eneo langu na katika Jimbo langu mradi wa REA Phase I hatukupata, lakini tukapata mradi wa REA Phase II, lakini kwa bahati mbaya hatukuweza kupata umeme hata kijiji kimoja katika REA II. Basi tunaomba vijiji vyote hivi viingizwe kwenye REA III kwa maana ya vijiji vyote 33, tunaomba mtusaidie kupata umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari kuna Shirika ambalo linafanya kazi kule kwa ushirikiano wa Serikali, Shirika la CEFA ambalo limeingiza vijiji viwili, sasa tatizo bado ni kadri ya mkataba ile asilimia ambayo Serikali ilitakiwa ichangie naomba tujitahidi tuweze kuwapatia lile Shirika ili liweze kuendelea na kuhakikisha kwamba linasambaza umeme kwenye vijiji vingine ambavyo tayari nguzo zimechomekwa lakini bado nyaya hazijafungwa na hawajazambaza umeme, kwa hiyo niombe hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niombe kupitia ile mradi ambao wa kwanza ulikuwa TANESCO, ile Gridi ya Taifa iliyowenda mpaka vijiji vile vya Lupembe na Igombora, basi kuna baadhi ya vijiji vilirukwa haukushushwa umeme, umeme umekatiza tu umepita katikati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mara nyingi wananchi wamekuwa wakilalamika kwamba umeme umepita kwenye vijiji vyao, lakini vijiji hivyo havina umeme au vitongoji mbalimbali ambavyo umeme umepita juu haujashushwa. Tuombe tunapopeleka umeme kwenye maeneo hayo au kwenye maeneo mengine tuhakikishe kwamba yale maeneo ambako umeme unapita basi wananufaika na nishati ya umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe pia bei ya umeme ilivyo sasa hivi pamoja na kwamba tumepunguza kutoka kwenye asilimia 1.5 mpaka 2.4 bado bei hizi ziko juu. Kuna baadhi ya wananchi wengi wanashindwa kulipia gharama hizi, tuangalie uwezekano wa kupunguza gharama za umeme angalau zishuke kabisa kutoka kwenye ile asilimia ziende chini kidogo ili wananchi wengi wa kipato cha chini waweze kununua na kutumia umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ilivyo sasa hivi, tunasema mazingira yanaharibika kwa kutafuta mkaa, wananchi wanatumia mkaa walio wengi lakini pia wanatumia kuni katika kupata nishati. Tukishusha bei ya umeme ukawa wa gharama ndogo au ukawa gharama ambayo wananchi wa kipato cha chini wanaweza wakaununua basi yale madhara ya misitu kwa maana ya kutafuta nishati ya mkaa na kupata kuni yatapungua. Wengi wao watahamia kwenye umeme kwa kuwa umeme utakuwa una bei ndogo, utakuwa wa bei rahisi na wataweza kununua umeme na kwa upande mwingine tutakauwa tunapunguza madhara ya kupotea kwa misitu, tutakuwa tunapunguza uharibifu wa mazingira kupitia kutumia hizi nishati za mkaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba tujitahidi tuweze kuhakikisha kwamba umeme unapungua uwe na bei ndogo ili tuweze kuokoa mazingira yetu na misitu yetu ambayo kila siku tani za miti zinakatwa kwa ajili ya kupata nishati hii ya kupikia kwa maana ya mkaa na kuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme kwamba huduma ya umeme hii lazima tufikirie kuisambaza hasa kwenye maeneo yenye taasisi kama vile shule, maeneo ya Hospitali,na maeneo ya huduma muhimu za binadamu. Kwa hiyo lazima tufikire hilo pia tunasema kwamba tunataka shule zetu ziwe na E-schools, tuwe na E-learning ni lazima tuweze kuhakikisha kwamba tunakuwa na umeme ili mipango ya kuwa na E-learning, E-schools kwenye shule zetu uweze kukamilika. Kwa hiyo, tunaomba tupeleke pia kwenye huduma hizi za kielimu na huduma nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naona kuna Waheshimiwa Wabunge wengi wamelalamika sana juu ya kuweka vinasaba kwenye nishati ya mafuta. Kwanza lazima tujiulize sababu zipi zilizosababisha Serikali iweze kuhakikisha kwamba inaweka vinasaba. Ni kutokana na kwamba kulikuwa na uchakachuaji wa mafuta kwa kiasi kikubwa, magari yamekuwa yakiharibika, pampu za magari zikiharibika mara kwa mara na baada ya sisi wananchi kulalamika na Wabunge tukaja tukaa na tukajadili, tukaamua kwamba tupitishe sheria ya vinasaba. Kwa hiyo, vinasaba hivi ni muhimu, naomba Waziri na Baraza zima la Mawaziri viendelee, kama kuna matatizo madogo madogo basi yafanyiwe uchunguzi tuweze kuyatatua lakini sio kusimamisha hili suala la vinasaba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tumeona faida zake, udhibiti wa uchakachuzi wa mafuta umepungua lakini pia Serikali imekuwa inapoteza mapato mengi sana hasa kwenye mafuta yale yaliyopo on transit kama walivyosema wenzangu. Kwa hiyo, kwa kuweka vinasaba tunaweza tukabaini kwamba haya mafuta yamepitiwa na vinasaba, watu wanaokagua vinasaba na haya mafuta hayajapitiwa. Kwa hiyo, kwa kwa kufanya hivyo tutadhibiti upotevu wa kipato cha Serikali na hivyo Serikali itaweza kupata pato lake vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia hasara kubwa kama nilivyosema ya haya mafuta kulikuwa na wizi mkubwa sana wa mafuta ambayo yanakuwa kwenye on transit, kulikuwa na wizi mkubwa sana wa mafuta yaliyopo kwenye migodi. Kwa hiyo, kwa kufanya hivyo maana yake tutapunguza madhara ya wizi wa mafuta ambao ulikuwa unapelekea hasara kubwa hasa wenye migodi wenyewe, lakini kwa upande mwingine ulikuwa unapelekea hasara Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja kwa asilimia mia moja, ahsante sana kwa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami nianze kwanza kabisa kwa kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wa Ardhi, Nyumba na Makazi na Naibu Waziri wake na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa wanayofanya katika kutatua migogoro. Ni kweli migogoro imepungua sana ukilinganisha na siku za nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nianze na jambo moja hasa kuhusu property tax (kodi za majengo). Kodi hizi ni kubwa mno ukilinganisha na kipato cha wananchi hasa wastaafu na wale wenye kipato cha chini, inakuwa vigumu sana kwao kuilipa. Kwa mfano, mfanyakazi ambaye amestaafu alikuwa anapata kima cha chini amejenga nyumba yake yenye thamani ya shilingi milioni 40, anatakiwa kulipia kodi Sh. 46,000 kwa mwaka na ukigawa kwa mwezi ni kama Sh. 3,840 hivi, kodi hii ni kubwa. Kwa hiyo, tuombe Serikali ijaribu kuangalia uwezekano wa kupunguza kodi hizi za majengo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Sheria ile ya Ardhi hasa inayosema juu ya vyanzo vya maji kwamba mwananchi haruhusiwi kujenga mita 60 kutoka kwenye chanzo cha maji au kwenye kingo za mto. Hii sheria kwenye maeneo mengine hasa ya nyanda za juu (highlands) haitusaidii sana au inawaathiri sana wananchi. Kwa mfano, utakuta kuna milima midogo na kutoka mlima mmoja mpaka mwingine au kutoka bonde mpaka bonde, ukipima kutoka kwenye kingo za maji mpaka unapoishia mlima utakuta unafika kwenye mlima pale katikati kwenye kigongo cha mlima. Kwa hiyo, maana yake hilo eneo utakuta milima miwili au mitatu hawaruhusiwi wananchi kujenga maeneo hayo kwa sababu ya sheria hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Sheria hii ya Ardhi iwe applicable kwenye baadhi ya maeneo lakini kwenye maeneo ya milimani angalau waweze kupunguziwa zile mita 60 ziende kwenye mita 30 au 20 hivi ili wananchi nao waweze kujenga kwenye maeneo hayo vizuri zaidi kama ilivyo katika maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia jambo lingine ni migogoro hii ya mipaka. Kwangu kule kuna migogoro hasa kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Njombe na Halmashauri ya Jimbo la Mlimba. Naomba ule mgogoro wa mpaka kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Njombe kwa maana ya Jimbo la Lupembe na Jimbo la Mlimba uweze kutatuliwa haraka ili tuendelee kufanya shughuli za kimaendeleo. Kwa sababu ukiwauliza watu wa Njombe wanasema mpaka wao unaenda mpaka kwenye mto, lakini watu wa Mlimba nao wanasema hapana siyo mto ni ndani zaidi ya Njombe. Kwa hiyo, bado ule mgogoro unatuathiri sana katika maendeleo kwa hiyo tunaomba muutatue ili tuweze kujua mpaka halisi upo sehemu gani maana umedumu kwa muda mrefu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la hizi nyumba za National Housing, bei yake ni kubwa mno. Lengo la nyumba za National Housing tukimrejea Mwalimu Nyerere alikuwa na lengo la kuwasaidia watu maskini na wafanyakazi na watu wenye kipato cha chini. Sasa hivi zile nyumba mwananchi wa kawaida au mfanyakazi wa kima cha chini hawezi kununua, nyumba ya vyumba viwili kwa shilingi milioni 70, kwa kweli hawawezi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuombe wajaribu kurekebisha baadhi ya taratibu, inawezekana pengine ni Sheria ya Manunuzi ndiyo inayopandisha bei, basi tuirekebishe ili wananchi hata wale wa kipato kidogo waweze kunufaika. Ilivyo sasa hivi hizi nyumba za National Housing na hata zile zinazojengwa na NSSF sehemu kubwa wanaoweza kununua ni watu wenye kipato kikubwa, ni matajiri na wafanyakazi wenye kipato kikubwa ndiyo wanaoweza kumudu kununua nyumba hizi tofauti na lile lengo hasa la msingi la kujenga hizi nyumba kwa ajili ya watu wa kipato cha chini. Otherwise hawa watu wenye kipato cha chini wataendelea kuwa wapangaji na hawataweza kumiliki nyumba zao kwa sababu bei ya nyumba hizi ipo juu mno. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe pia Idara ya Ardhi kwenye Jimbo langu la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, hatuna Afisa Ardhi Mteule. Kwa hiyo, kunapotokea migogoro ya ardhi tunashindwa kuitatua wakati mwingine inabidi twende kwa wenzetu wa Halmashauri ya Mji waweze kutusaidia kwenye baadhi ya maeneo. Kwa hiyo, tuombe Halmashauri zote ambazo hazina Maafisa Ardhi Wateule basi waajiriwe ili tuweze kutatua migogoro ya ardhi na mipaka ambayo inajitokeza huko kwenye Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niseme jambo moja juu ya ucheleweshwaji wa hati miliki, inachukua muda mrefu sana kupata hati miliki ya ardhi au ya viwanja. Tunaomba basi kwa kuwa sasa hivi ni ulimwengu au ni wakati wa sayansi na teknolojia, basi ziwe printed haraka ili zisiwe zinachukua muda mrefu sana ili wananchi waweze kunufanika na hili suala la kupata hati miliki kwa maana ya mashamba madogo na makubwa na viwanja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwangu wananchi walishapimiwa ardhi ili kupata hati miliki za mashamba ya chai, lakini imechukua muda mrefu sana na ukiuliza sababu wanasema hatuna Afisa Ardhi Mteule ambaye anaweza akasaini hati hizo. Sasa hivi baada ya kumwona Afisa Ardhi wa Mji ndiye anatusaidia angalau ku-process zile hati miliki ili kuwawezesha wananchi wangu wa Lupembe kupata hati zao kwa ajili ya mashamba yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa nafasi hii, naunga tena mkono kwa mara ya pili kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru kwa kupewa nafasi hii kuchangia kwenye Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2018/2019. Nianze kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambazo anazifanya katika utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015. Niwapongeze Mawaziri kwa kazi kubwa ambazo wanazifanya na wanashirikiana na Rais kuhakikisha kwamba Ilani ya Chama cha Mapinduzi inatekelezwa vizuri, niwapongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa jinsi anavyosimamia shughuli nzima za mapato na matumizi kwa maana ya uchumi wa nchi hii na amekuja na hotuba nzuri ambayo inaleta matumaini kwa Watanzania, nikupongeze sana Waziri na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuiangalia sekta ya kilimo. Sekta ya kilimo ndiyo sekta ambayo ni mhimili wa uchumi wa nchi yetu na sekta hii inachangia takribani nusu ya pato la Taifa letu kwa maana ya uchumi wa Taifa. Hivyo basi, Watanzania wengi ndio walipo huko, wameajiriwa huko wanafanya shughuli za kiuchumi, kwa hiyo ni lazima tuiangalie kwa namna ya pekee sana ili angalau iendelee kuchangia zaidi hata kuliko kuishia kwenye nusu pengine iende mpaka kwenye robo tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja ni kwamba katika kilimo kuna mazao ya aina mbili, kuna mazao ya chakula na mazao ya biashara. Niseme kidogo juu ya mazao ya biashara, tuna pamba, tumbaku, kahawa na mazao mengine kama chai. Mazao mengi ya biashara yanapewa ruzuku na Serikali na angalau sasa hivi tunaona mazao mengi yanapata bei nzuri, tukiangalia kwenye korosho bei ilikuwa chini lakini sasa hivi imepanda kwa sababu ya ruzuku ambayo inatolewa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, bado kuna mazao mengine hatujayapa kipaumbele wakati mazazo hayo yanaweza yakatuingizia fedha nyingi sana za kigeni kama tukiamua kuwekeza huko na kuhakikisha kwamba tunawasaidia wakulima wetu waweze kuzalisha kwa wingi na kwa ubora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue mfano wa zao la chai, sijaona likitiliwa mkazo sana, ikumbukwe kwamba zao hili katika miaka ya 1990 kurudi nyuma ndiyo zao ambalo lilikuwa linaingiza fedha nyingi sana za kigeni. Lilikuwa ni zao ambalo ni mtetea uchumi mzuri sana lakini sasa hivi ni kama tumelitelekeza hivi bado halisimamiwi vizuri na wakulima bado bei zao zipo chini na hakuna usimamizi mzuri kutoka kwa mkulima anavyoichuma chai kupeleka kiwandani na hatimaye kwenye soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkulima hajui chochote, akishauza chai yake pale kwenye banda au kwenye kituo chake anachouzia hajui chochote nini kinapatikana mwisho wa siku. Kwa hiyo, ufuatiliaji katika chain nzima ya ukamilishaji wa zao la chai haupo na matokeo yake bei ya chai imeendelea kuwa chini, sasa hivi inalipwa kati ya Sh.230/= mpaka Sh.250/= ukilinganisha gharama za uzalishaji wa zao hili ni kubwa kuliko kile anachokuja kukipata mkulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majani mabichi sasa hivi kama nilivyosema ni Sh.230/= mpaka Sh.250/=, lakini gharama za uzalishaji zinazidi Sh.450/=. Ukiangalia kwa nchi za wenzetu, ukiangalia kwa mfano Kenya, mwaka jana kwenye kilo moja ya chai ambayo tayari ni majani makavu waliweza kupata kwa kila kilo dola 266, kwa hiyo ukii-convert katika fedha za Kitanzania pengine ni kama Sh.5,000/= hivi na zaidi. Kwa hiyo, kumbe inawezekana tukiisimamia vizuri hii sekta, tukisimamia vizuri zao linaweza likatuletea uchumi mzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali ijitahidi kuhakikisha kwamba kwanza inaisimamia Bodi ile ya Chai vizuri ili bei ziweze kupanda kadri ya muda unavyozidi kwenda. Ukiwauliza wenyewe wanaozalisha chai, wale wanao-process chai, wanasema haina faida lakini ukiuliza nje ya nchi kule wanakouza chai wanasema wanauza kwa bei nzuri sana. Kwa hiyo, tunajiuliza sisi wakulima wa chai kuna nini pale katikati, kwa nini bei ya chai haipandi. Bei iliyopo sasa hivi kwa mara ya mwisho iliongezwa mwaka 2012, mpaka sasa hivi bado bei ni ileile. Tunasikia tu kwamba hivi karibuni Bodi ya Chai itaenda kutangaza bei elekezi, basi tuombe hiyo bei itangazwe mapema ili wakulima wajue na waweze kupata faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna tozo ilitolewa kwenye chai, tozo ya shilingi mbili; lakini wakulima hawaioni hiyo, haiendi kwa wakulima mpaka sasa hivi. Kwa hiyo niiombe Serikali, nimwombe Waziri wa Kilimo ajaribu kusimamia ili kuhakikisha kwamba kila tozo zinavyokuwa zimeondolewa lazima zi-reflect wakulima tu na zionekane kwa wakulima ili waone kwamba zile tozo zina tija kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikuombe sana tusimamie hili na tusaidie hili, ili wananchi hawa waweze kupata fedha hizo ambazo zinawasaidia kusomesha watoto wao, zinasaidia kujenga nyumba nzuri na zinasaidia kufanya mambo mengine makubwa na mwisho wa siku kiuchumi kama wa wakulima unakuwa, lakini uchumi kama nchi pia unaongezeka. Kwa hiyo ni lazima tuanze kusimamia haya mazao tunayofikiri ni madogo ili baadaye kwa ujumla wake ndiyo yaweze kukuza uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema viwanda, viwanda vitaongezeka kama uzalishaji utaongezeka lakini ilivyo sasa hivi kwenye zao la chai ni kama watu wanakata tamaa kwa hiyo hata viwanda havitakuwepo. Tukiongeza usimamizi katika uzalishaji wa zao la chai, naamini hata wakulima watafurahi, watazalisha kwa wingi, mashamba yataongezeka na ajira nyingi zitaongezeka kupitia mashamba na viwanda na viwanda vitaongezeka. Kwa hiyo, wazo la kufikia kwenye uchumi wa viwanda tutafika kama mazao haya ya biashara yanasimamiwa vizuri kuanzia mwanzoni mkulima anapozalisha lakini mpaka mwisho wa soko mkulima aonekane kwamba kuna faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa kunakuwa kuna malipo ya pili baada ya kuuza yale majani mabichi lakini wananchi wengi hawayapati haya. Kwa mfano, wakulima wangu wa Lupembe kule hawapati mauzo ya pili au ile fedha inayokuja baada ya kuuza majani makavu, wakilipwa tu yale majani mabichi inakuwa ni mwisho wa malipo. Kwa hiyo, niiombe Serikali, niombe Wizara isimamie vizuri jambo hili ili wakulima hawa waweze kuongeza uzalishaji na wakione kilimo kama kina tija na mwisho wa siku tutaongeza uchumi wa nchi lakini pia tutakuwa tumeongeza Pato la Taifa kupitia hili zao la chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nije kwenye upande wa kilimo cha mazao ya chakula, niseme kidogo kuhusu zao la mahindi. Kama walivyosema wenzangu kwamba zao la mahindi kwetu sisi sio zao tu la chakula bali ni zao la biashara. Kuna wananchi wanalima mahindi kwa ajili ya chakula, lakini pia kwa ajili ya kuuza kuweza kupata fedha kwa ajili ya kusomeshea watoto wao. Hivi sasa baada ya hili zuio, kama walivyosema wenzangu zuio la kuuza mahindi nje ya nchi, wakulima wetu wamebakiwa na mahindi na wengine wanauza kwa bei ndogo sana kati ya Sh.3,000/= mpaka Sh.5,000/-.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, ukipiga hesabu ya gharama za uzalishaji wa zao la mahindi na bei wanayouzia mahindi kwa gunia kwa maana ya Sh.20,000/= mpaka Sh.25,000, bei hiyo inawapa hasara kubwa sana. Kwa hiyo sasa hivi wanashindwa kununua mbolea ambapo msimu wa kuanza kilimo cha mahindi ndiyo huu umeanza, sasa hivi wameshaanza kulima mashamba, mwisho wa mwezi huu wanatakiwa waanze kupanda. Hata hivyo, hawawezi kulima vizuri na kupanua kilimo chao kwa sababu hawajauza mazao yao kwa bei nzuri na hawajapata fedha za kutosha za kuweza kununulia hizi mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Wizara, mbolea imeshafika na bei imepungua tumeshaiona, lakini wakulima wetu hawawezi kununua zile mbolea kwa sababu hawana fedha za kutosha. Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Serikali kwa ujumla wakae wajaribu kulitafakari hili na wajaribu kuangalia jinsi gani tutawasaidia wale wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru Serikali imenunua kupitia Hifadhi ya Chakula (NFRA) imenunua mahindi, lakini imenunua kiasi kidogo sana. Mahindi yapo mengi, sisi Waheshimiwa Wabunge na viongozi wengine tulihamasisha wananchi walime kiasi cha kutosha ili waweze kuuza tuki-refer soko la mwaka jana, kwamba mkiuza mtauza kwa bei nzuri na mtapata faida kubwa. Hata hivyo, sasa hivi ilivyo inaonekana kama sisi Waheshimiwa Wabunge na viongozi wengine tulikuwa tunawadanganya. Hivyo, wawakilishi wa wananchi na viongozi wengine tunalaumiwa kwa sababu wananchi hawana sehemu ya kupeleka yale mahindi na kuweza kuuza ili waweze kupata fedha na kuweza kufanya mambo yao mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe Waziri, hebu wajaribu kuliangalia kwa jicho la pekee ili wajaribu kujadili na tuweze kuangalia jinsi gani tutaweza kuwasaidia wale wakulima wetu waweze kuuza yale mazao yao lakini wauze kwa bei nzuri. Ikiwezekana, wakifungua mipaka inakuwa rahisi kwetu kwa sababu wafanyabiashara wakubwa wanakuja na bei inapanda kwa sababu kunakuwa na ushindani wa ununuzi wa mahindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimwombe sana Waziri na niiombe pia Serikali kwa ujumla wajaribu kutafakari hili na tuangalie jinsi gani tutaweza kuwasaidia wale wakulima wa mahindi waweze kuuza mazao yao ili wakishauza waweze kupata fedha za kununulia mbolea, lakini pia wapate fedha za kuweza kusomeshea watoto wao. Januari shule zinafungua wanategemea wauze hayohayo mahindi, watashindwa kupeleka watoto wao kwa sababu ya ada na michango mbalimbali ambayo inatakiwa kwenye shule kwa kule watakakokuwa wamepeleka watoto wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme juu ya miundombinu. Kilimo au shughuli zote za maendeleo zinategemeana sana na miundombinu. Kwa hiyo miundombinu kama barabara, reli, mambo ya viwanja vya ndege na mambo mengine vikiboreshwa vizuri ndiyo vinasaidia kukua kwa uchumi. Niipongeze Serikali na nimpongeze Rais kwa jinsi ambavyo anapigania uboreshaji wa barabara, uboreshaji wa miundombinu ya reli na uboreshaji wa viwanja vya ndege, ni jambo jema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna baadhi ya maeneo bado uboreshaji haujafanyika sana. Kwa mfano kwenye Jimbo langu mimi la Lupembe; nishukuru kwamba barabara kwa maana ya zile za vumbi zinapitika sehemu kubwa, lakini kuna tatizo la barabara ile ya lami ambayo ilitakiwa ijengwe. Ilikuwa ni ahadi kwenye Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015, kwamba Barabara ya Kibena – Lupembe – Madeke itajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii tunaitumia sana sisi wananchi wa Lupembe kwa maana ya kusafirisha mazao mbalimbali, hasa mizigo mizito kama ya mbao, kusafirisha mizigo kama ya nguzo za umeme na kusafirisha mazao ya mahindi, maharage, matunda – mananasi, maparachichi na mazao mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii barabara ikifika wakati wa kifuku huwa inakuwa ni ngumu sana kusafirisha mizigo kama hii. Wakati wa kifuku, wakati inaisha mvua ndivyo mazao haya yanapotolewa. Kwa hiyo, niombe katika bajeti ya mwaka jana, mwaka 2016/2017 zilipitishwa bilioni nane lakini bado haikutangazwa na mwaka huu tumepitisha bilioni mbili kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami lakini bado haijatangazwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe Waziri mwenye dhamana atusaidie kutangaza barabara hii ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami ili tuweze kuhakikisha kwamba mazao yaliyopo kule kwenye maeneo yetu, kule vijijini, yaweze kusafirishwa kuweza kufikia soko. Maana yake nguzo kwa kutumia barabara za vumbi zikishapita gari ndani ya wiki moja au mbili tayari barabara zimeharibika, lakini ikiwa lami tunaamini kwamba mazao haya yatasafirishwa na uchumi wa maeneo haya utakuwa lakini mwisho wa siku, uchumi la Lupembe utachangia uchumi wa Taifa na uchumi wa nchi kwa ujumla utakua kupitia uzalishaji unaofanyika kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niseme juu ya umeme. Nnashukuru sana kwamba mpango wa umeme, hasa umeme vijijini, unaendelea vizuri kwa maana tumeshaanza kuona baadhi ya maeneo kuna nguzo zinachomekwa, lakini kwetu sisi ujenzi wa line bado
haujaanza. Tunashukuru kwamba kuna line ile ya Makambako – Songea, wameshapitisha line lakini bado hawajaanza kusambaza umeme kwenye vile vijiji kadiri tulivyoahidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba, katika mipango ya fedha ya Serikali hii nayo tuiwekee kipaumbele ili sasa umeme huu uweze kwenda huko vijijini, vijiji vingi viwe na umeme. Tunajua kwamba umeme unachochea maendeleo, unachochea shughuli za kiuchumi nyingine kwa sababu tukiwa na umeme itakuwa rahisi kuanzisha viwanda vidogovidogo, tukiwa na umeme itakuwa rahisi hata kusukuma maji. Kwa mfano, Lupembe maji yapo chini – kusukuma maji yaweze kupandisha majumbani na kuweza kufanyia shughuli mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo umeme una manufaa makubwa sana endapo vijiji vyetu hivi vitakuwa na umeme. Namwomba Mheshimiwa Waziri, hebu tupate utaratibu mzuri, maana yake sasa hivi ni kama haieleweki vizuri ni lini umeme utaanza kusambazwa. Tukipita huko tunaulizwa na wananchi kwamba mlituahidi umeme wa REA lakini hatuoni hata nguzo zikisambazwa kwenye vijiji vyetu zaidi ya ile line ambayo imepita inayokwenda Songea. Kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri atusaidie haya, katika mipango ijayo angalau maeneo haya ile mipango ambayo tumeipanga kwamba itatekelezwa kuanzia mwaka huu, wananchi waanze kuiona ikitekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nikushukuru sana na naunga mkono hoja iliyopo Mezani kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa uamuzi wake wa kizalendo na kijasiri wa kuzuia usafirishaji au utoroshaji wa madini nje ya nchi na makampuni haya ya madini. Nampongeza sana. Naomba Watanzania hasa Waheshimiwa Wabunge tunapokuwa kwenye mambo ya msingi yanayohusu nchi na maslahi ya nchi, ni muhimu sana kuungana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamepiga kelele hapa, wamelalamika kwamba wanaonewa, mara tutashtakiwa, lakini leo hii, mchana huu tumeshaona Mwenyekiti wa Makampuni ya Barrick amekuja kuomba msamaha kwamba fedha au madini waliyotorosha watarejesha hizo fedha na wapo tayari kujenga mtambo wa smelting wa kuweza kuyeyusha madini haya nchini. Kwa hiyo, nampongeza sana Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa uamuzi huo. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, tunapokuwa na mambo ya Kitaifa, tunapokuwa tunatetea jambo la kuhusu Taifa hili, kuhusu uchumi wa nchi hii na tunapotetea wanyonge wa nchi hii, ni muhimu sana kuungana. Tunapotengana Waheshimiwa Wabunge ndio tunapoteza na tunawakandamiza wale wenzetu wanaobaki kule ambao wametutuma tuwatetee. Naomba siku nyingine tujifunze kuungana na kuwa wazalendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kuleta hotuba nzuri ya Wizara yake. Ni hotuba ambayo inatuonesha kwamba tunaenda sasa kwenye uchumi wa kati, uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza kwa kuondoa hizi kodi na tozo mbalimbali. Nimeona mmeshaondoa tozo na kodi mbalimbali kwenye malighafi ambazo zinatumika kutengenezea vifaa vya walemavu. Zinapoingizwa toka nje, kodi zimepungua na kuondolewa kutoka asilimia 25 na sasa itakuwa asilimia sifuri. Nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii hakuna asiyejua, walemavu tunao wengi na kila siku walemavu wanaongezeka. Hata sisi Waheshimiwa Wabunge tuliopo humu ndani ni walemavu watarajiwa. Kwa hiyo, kwa kupunguza hii kodi na tozo kutoka kwenye asilimia 25 mpaka sifuri kutawezesha sasa viwepo viwanda vya kutengeneza au kuunganisha vifaa vile ambavyo wanatumia watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tutatoa ajira ambayo itasaidia vijana wetu waliopo hapa nchini, waweze kuajiriwa kwenye hivi viwanda vya uunganishaji au kwenye viwanda vile vinavyohusika na utengenezaji wa hivi vifaa ambavyo wanatumia walemavu. Nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Naibu wako kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, napongeza pia kwa kazi kubwa mliyoifanya kwa kuondoa kodi hasa kwenye mazao wanayozalisha wakulima wadogo wadogo. Wakulima wamekuwa wakipata shida sana na bei ya mazao imekuwa haipandi kwa sababu ya kodi nyingi ambazo wanawekewa hawa wakulima. Kwa hiyo, napongeza kwamba mmeondoa hizi kodi, naamini sasa wataweza kuuza kwa bei nzuri na hatimaye kupata faida kutokana na shughuli zao za kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja ambalo pengine tuliangalie vizuri. Kule Lupembe katika Jimbo langu, tuna kilimo cha miti; tunapanda miti na tunahamasisha watu wapande miti kama zao la biashara. Sasa inapofika wakati huyu mkulima ametunza miti yake, anaenda kuuza sokoni, anakutana na kodi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya kodi anayolipa anatakiwa kulipa transit pass ambayo inalipwa Serikali Kuu Sh.15,000/=, anatakiwa kulipa TP katika Halmashauri ambayo ni Sh.3,000/=, anatakiwa kulipa ushuru wa mbao ambao ni Sh.200/= kwa kila mbao, lakini pia anatakiwa kulipa ushuru wa leseni ya biashara ambayo ni Sh. 261,000/= kila mwaka, anatakiwa alipe kodi ya mapato ambayo ni Sh.1,500,000/= kwa mwaka, anatakiwa alipe leseni ya uvunaji ambayo ni Sh.261,000/= na vile vile anatakiwa akodi gari kwa Sh.3,000,000/= ili aweze kufikisha mzigo wake pale Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hizi kodi ni nyingi mno. Anaambiwa kwamba unapokuwa amelipa hizo kodi mbalimbali ni lazima awe na risiti ya EFD. Huyu mkulima amelima miti yake, ameungana pengine na wenzake au yeye mwenyewe ameamua kuipeleka sokoni ili aweze kupata bei nzuri. Anapopeleka sokoni anakutana na hiki kikwazo kwamba lazima awe na risiti ya EFD; huyu mkulima hana mashine, atapata wapi risiti ya EFD zaidi ya ile risiti ambayo inakatwa na Halmashauri na risiti nyingine za ushuru ambazo nimeziorodhesha hapa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuliangalia hili. Kwa kweli wakulima wa miti wa Njombe, Lupembe na maeneo mengine ya Njombe tunaozalisha miti, imekuwa ni kero kubwa sana kwao. Hebu Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango ajaribu kuziangalia hizi kodi ambazo wakulima wetu wamekuwa wakitozwa wanapokuwa wanasafirisha huu mzigo wa mbao ambao wameuzalisha.


Mheshimiwa Mwenyekiti, nijaribu kusema pia kodi moja ambayo ni kero kwenye maeneo mengi lakini pia na kwenye eneo letu sisi. Kuna hii kodi ya SDL (Service Development Levy) ambayo inatozwa kwa kutoa huduma; wanalipa kwenye mashule lakini pia wanalipa wafanyabiashara. Hebu tujaribu kutoa ufafanuzi mzuri na tujaribu kuwaelimisha na kutoa elimu ya kodi vizuri ili waweze kuielewa, maana ilivyo sasa hivi hawaelewi vizuri. Kwa mfano, kwenye shule wamekuwa wakitoa hizi kodi nyingine nyingi lakini pia wanalipa na hii kodi ya Service Levy na wakati huo huo wanatakiwa warejeshewe fedha zile kwa ajili ya kuendeleza mafunzo ya ufundi, lakini shule zimekuwa hazipewi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tujaribu kuziangalia hizi kodi na ikiwezekana tukae na hawa wenye shule na wafanyabiashara ili wasione kama ni kero. Waelimishwe vizuri, naamini wakielewa vizuri wataweza kulipa hii kodi vizuri bila tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kodi nyingine ambayo ni kodi ya uanzishwaji wa maduka ya madawa. Nawapongeza sana, imeshaondolewa, nayo ilikuwa ni kero kubwa; lakini mmesahau kodi ya uanzishwaji wa maabara. Maana duka la madawa linaendana na maabara. Kwa sababu kuwa na duka la madawa maana yake kuna Daktari ambaye kabla ya kutoa prescription anatakiwa aende kwenye maabara huyu mgonjwa akapime na akishapimwa arudi kuandikiwa dawa. Sasa kwenye maabara hamjatoa hizi kodi. Mpaka sasa hivi wanalipa kodi kwa maana ya uanzishwaji wa maabara Sh.330,000/= kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama basi ajaribu kuaingalia hii kodi pia, maana wenye maabara wanalalamika kwamba kwa nini wao wamesahaulika wakati wenzao wamepewa hilo punguzo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme juu ya maji vijijini. Wote tunajua Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakipiga kelele sana juu ya tatizo la maji vijijini. Maji yamekuwa yakipoteza muda mwingi sana wa akinamama na mabinti zetu kwenda kutafuta maji. Naomba katika ile Sh.40/= basi fedha hiyo iende kwa ajili kuongezea kwenye Sh.50/= ya zamani ili iwe Sh.90/= ili usambazaji wa maji uweze kuongezeka na hatimaye mama zetu hawa wasipoteze muda mwingi kwenda kutafuta maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anaweka mambo haya sawa tujue hii Sh.40/= inaenda wapi? Wengine wamelalamika kwamba Sh.40/= ni kubwa inaongezea wananchi gharama. Wamesema wasafirishaji hapa kwamba haiongezi chochote kwa maana ya gharama za nauli. Kwa hiyo, kama haiongezi chochote na watumiaji wa mafuta ya dizeli na petroli ni watu wenye magari au ni watu ambao wana bodaboda, naamini kwamba wana uwezo wa kustahimili kulipa hii Sh.40/= ambayo imeongezwa kwenye tozo za mafuta ili wananchi wetu waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni juu ya miradi ya umeme kwa maana ya REA. Naipongeza sana Serikali kwa kuanzisha utaratibu huu kuhakikisha kwamba kila kijiji sasa kinapata umeme. Nashukuru, nimeona kwenye mpango katika vijiji vyangu vyote; Vijiji vya Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe vimeshawekwa kwenye mpango wa kupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba watakapofika wasisahau maeneo au kusiwepo na vitongoji vitakavyopitilizwa bila kuwa na umeme au havishushiwi umeme kwenye eneo fulani ili kusiwe na ugomvi au kusiwe na malalamiko ya wananchi ambao hawajapata umeme kwenye Vitongoji. Kwa hiyo, naamini Serikali yangu, naamini Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini yupo, basi mtahakikisha kwamba kila kijiji na kila kitongoji kinakuwa na umeme ili wananchi wetu waweze kutumia umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo…
(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata fursa kwa ajili ya kuchangia hii Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani.

Kwanza nianze kuishukuru sana Serikali hasa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii ya Mambo ya Ndani na maaskari wote kwa namna walivyodhibiti mauaji ya watoto katika Mkoa wa Njombe na Simiyu, nawashukuru sana. Naomba Mwenyezi Mungu aendeee kuwabariki na aendelee kuwalinda ili tuweze kudhibiti tabia za namna hii na hatimaye Watanzania wasiweze kupotea kupitia mauaji mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumshukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa namna wanavyofanya kazi zao hasa katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani. Kazi ni ngumu, kubwa sana, inahitaji weledi na pia inahitaji ustaarabu mkubwa. Nashukuru Mwenyezi Mungu anawatia nguvu wanaendelea kumudu na hatimaye tunaona matokeo ya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie juu ya makazi. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kutoa zile bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba 400 za askari wetu nchini. Tumeona zimegawanywa kwenye baadhi ya mikoa, kuna mikoa inapata nyumba 88 na mingine nyumba 20 na mgawanyo umeenda karibu kila mkoa ambao una upungufu mkubwa sana wa nyumba za askari wetu. Mkoa wa Njombe nimpongeze Mheshimiwa Rais ametupa nyumba 20 kwa ajili ya askari wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, askari wetu wanafanya kazi kubwa sana usiku na mchana. Nashangaa hata wakati mwingine watu wanavyowabeza, kazi wanazofanya maaskari wetu ni kubwa sana, wanatulinda usiku tukiwa tumelala, wanalinda maduka mbalimbali, maduka yetu na mali mbalimbali za wananchi wa Tanzania, lakini pia wanatulinda hata sisi Wabunge tuliomo humu ndani. Tunaweza kuongea kwa amani na tukaishi kwa amani humu ndani na tuna uhakika ni kwa sababu askari wetu wametuzunguka huku wanatulinda. Kwa hiyo wanafanya kazi kubwa, hata wanapokosea tutumie maneno mazuri kwa sababu ni binadamu na wakati mwingine sisi wenyewe tunawakwaza na ndiyo maana wakati mwingine wanaghafilika au wanachukua hatua ambazo kidogo kama binadamu wakati mwingine wanapotoka taratibu kwa sababu ya namna sisi wananchi ambao wanatulinda usiku na mchana, wanatutumikia muda wote lakini wakati mwingine tunageuka kuwapiga mateke, tunageuka kuwatukana na kuwapa lugha mbayambaya na matusi mbalimbali. Kwa hiyo niombe tuwaheshimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana bado maeneo mengi, mikoa mingi, nyumba za askari haziridhishi na wakati mwingine huwa wanaenda kazini wakiwa na frustrations ndiyo maana tunasikia wakati mwingine maaskari wanajiua, wanajipiga risasi kwa sababu ya frustration ya kukosa makazi. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri pia niiombe Serikali kwa utaratibu huu ambao Mheshimiwa Rais ameuanza angalau tuanze kujenga nyumba za maaskari hawa kila mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda katika Mkoa wa Njombe kwa mfano, Kituo chetu cha Polisi cha Wilaya pale ni cha zamani sana, ukiangalia hata jengo la kituo lenyewe ni la zamani. Kwa hiyo haiendani na hali halisi ya hatua ilipofikia kwa maana ya ngazi iliyofikia kile kituo. Kile kituo sasa hivi kinatumika kama kituo cha Mkoa lakini hadhi ya kituo chenyewe sio nzuri. Nyumba zile ni chakavu, lakini ukiangalia hata makazi ya maaskari kwa kweli ni duni sana. Kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri tuliangalie hili jeshi, tuangalie maaskari wetu wa Mkoa pale Njombe angalau wapate nyumba. Kukaa mitaani sio nzuri sana. Wakati mwingine wanakaa mitaani wanapanga nyumba na wakati mwingine wanaweza kuwa wanapanga nyumba na mhalifu. Inakuwa ni vigumu sana kumdhibiti huyu kwa sababu wakati mwingine wengine wanashawishika, wanaweza wasifanye kazi vizuri kwa sababu ya mazingira wanayokaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wanapokaa mitaani maisha yao yanakuwa hatarini kwa sababu akishajua kwamba askari fulani ndiye aliyenikamata anaweza akamdhuru anaporudi kutoka kwenye shughuli zake ule usiku au anapoamka asubuhi kwenda kufanya shughuli zake zile. Kwa hiyo wakiishi sehemu moja, wakiishi kwenye nyumba nzuri za Serikali watafanya kazi zao vizuri na hatimaye watakuwa na morale ya kufanya kazi kwa sababu wanaishi kwenye makazi mazuri. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Kangi na Naibu Waziri na Makatibu Wakuu, nafikiri wawasiliane nao vizuri hawa ili baadaye ikiwezekana bajeti ya makazi iweze kuongezeka na hatimaye maaskari wetu waweze kupata nyumba bora, waweze kuishi vizuri na waweze kuhamasika katika utendaji wao wa kazi wa kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye Jeshi la Magereza. Ni kweli Jeshi la Magereza wanafanya kazi kubwa lakini ukiangalia kwenye bajeti yao, Fungu lao namba 29, bajeti yao ni ndogo sana kwa hiyo ukomo wao ni mdogo. Hebu tupanue, tuongeze ukomo wa bajeti ya askari magereza kwa Jeshi la Magereza ili waweze kutekeleza majukumu yao vizuri. Wameeleza Waheshimiwa Wabunge hapa kwamba kuna shida ya sare za maofisa, hawana sare walio wengi, lakini pia ukiangalia hata maaskari hawana sare, ukiangalia Jeshi la Magereza hawana na wafungwa wetu sare zao nyingi zimechakaa. Kwa hiyo tukiongeza ukomo wa bajeti wataweza kumudu kutekeleza majukumu yao, lakini wataweza kununua vifaa na mavazi ambayo wanatakiwa wayanunue kwa ajili ya askari wetu lakini pia kwa ajili ya maafisa wetu na kwa ajili ya wafungwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana hili litiliwe mkazo ili wafungwa wetu, pamoja na kwamba wanakuwa wamefungwa lakini wana haki ya kupewa zile sare. Vilevile maafisa wana haki ya kupewa sare zao na maaskari wana haki ya kupewa sare zao, kwa hiyo tuwatekelezee hii haki ya msingi ya angalau ya kupewa nguo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amekuwa akisema mara nyingi kwamba Jeshi la Magereza waanzishe utaratibu wa uzalishaji. Kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri aweze kulisimamia hili. Kwanza tuya- identify magereza yetu yalipo, tuzi-identify fursa zilizopo katika magereza haya. Tujue kwamba kama ni Dodoma kuna fursa ipi wanaweza wakaifanya na mwishowe wakazalisha. Kama ni Njombe au mikoa kwa mfano yenye mvua nyingi tunaweza tukaanzisha shughuli za kilimo. Kwa hiyo kwenye mikoa hii tuanzishe shughuli za kilimo, lakini hatuwezi kuanzisha shughuli za kilimo bila kupeleka matrekta ya kulimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Kangi akae na wataalam wake wajaribu ku- identify maeneo yalipo magereza haya tuangalie ni shughuli gani wanaweza wakazifanya na hatimaye magereza yasiwe tegemezi. Serikali inatumia fedha nyingi sana kwa ajili ya kuwalisha wafungwa, lakini kumbe tukianzisha shughuli watakuwa wanazalisha na hatimaye kuipunguzia gharama Serikali ya kuwatunza hawa wafungwa wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, kwenye gereza la Idete, kinaweza kuanzishwa kilimo cha umwagiliaji cha mpunga na wakazalisha, halafu huo mpunga au mchele ukasambazwa kwenye magereza mengine, kwa hiyo badala ya kununua chakula basi wakapewa chakula kupitia magereza mengine. Pia kwenye magereza ambako hakuna uzalishaji tunaweza kuanzisha shughuli kama za useremala, kwa mfano, tumesema kwamba hapa Dodoma Msalato tutaanzisha useremala, basi uanze haraka ili waweze kuzalisha hizo bidhaa na waweze kuuza na hatimaye majeshi yetu yaweze kujitegemea kupitia hizo shughuli za kilimo. Kwa hiyo, tukifanya hivyo tutapunguza gharama kubwa ambazo tunazitumia kuwalisha hawa wafungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ili tuweze kupunguza msongamano wa wafungwa magerezani tuanzishe utaratibu wa adhabu mbadala. Badala ya wote kuwapeleka ndani, kwa mfano, wafungwa wanaokuwa na adhabu ya miezi sita, mwaka mmoja, hawa wanaweza wakatafutiwa shughuli, wakafanya shughuli za maendeleo, wakashiriki kwenye shughuli hizi za ujenzi kwa kuwa sasa hivi jeshi la magereza linashiriki kwenye shughuli za ujenzi na tumeona kazi zao wanafanya vizuri. Tumeona wamejenga hizo nyumba hapo za Mji wa Serikali. Kwa hiyo, kumbe tunaweza tukawatumia hawa wafungwa wale ambao wana vifungo vifupi, badala ya kupelekwa gerezani, wao wakapewa kazi ya kufanya kama vile kushiriki kwenye kazi za ujenzi na hatimaye tukapunguza gharama, tukapunguza msongamano…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia kwenye hotuba ya Waziri. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa namna anavyosimamia suala la elimu na idadi ya wanafunzi wameongezeka kutokana na uamuzi wake wa msingi kabisa kuhakikisha kwamba wanafunzi wote wanasoma bure hasa elimu ya msingi kuanzia awali mpaka kidato cha nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze sana Profesa Ndalichako, Waziri wa Elimu, Naibu Waziri wake, Naibu Waziri wake Mheshimiwa Ole Nasha, Katibu Mkuu wa Wizara hii ya Elimu na Manaibu Katibu Wakuu wote na watendaji wote kwa namna wanavyofanya kazi kwa weledi lakini pia kwa kujituma kuhakikisha kwamba kiwango cha elimu kinaongezeka nchini, niwapongeze sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie kidogo kuhusu suala la kwanza juu ya mikopo ya wanafunzi hasa mikopo ya elimu ya juu, kuna tatizo kubwa sana sasa hivi pamoja na kwamba wigo wa mikopo umeongezeka wanafunzi wengi wanapata mikopo lakini bado kuna idadi kubwa ya wanafunzi wengi wanakosa mikopo na hatimaye wengine kuacha kabisa kuendelea na masomo ya Chuo Kikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wengi wanaotoka vijijini maeneo ya vijijini wanakuwa wamedahiliwa, lakini wakifika Chuoni, kutokana na masharti yaliyopo au vigezo vilivyopo basi wanakosa na mwisho wa siku wanarudi tu vijijini na kuendelea na maisha pengine kufanya shughuli nyingine kuacha kabisa kuendelea na masomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Wizara lakini pia nishauri Serikali, nafikiri sasa tuanzishe utaratibu, kwa kuwa wanapewa mkopo na wanapewa na unaitwa mkopo siyo kwamba wanapewa bure tu, ni hela ambazo wanatakiwa warejeshe baada ya kumaliza masomo yao. Hivi ni kwa nini sasa tusiwe na utaratibu kwamba kama mwanafunzi amedahiliwa kwenda kuanza Chuo Kikuu apewe tu mkopo kama tunavyosema mkopo, akimaliza basi abanwe alipe na kwa kuwa sasa tunaona hata makusanyo ya mkopo yanaongezeka kutokana na jitihada zao, basi tuombe sasa tuwape mikopo wote wanafunzi ambao wanakuwa wamedahiliwa kwenda Chuo Kikuu, kuliko ilivyo sasa hivi, utakuta kwamba watoto wengi wa maskini, sisi tunaotokea maeneo ya vijiji Wabunge tunajua, tunajua namna gani watoto wanavyohangaika huko, kila siku watoto wamejaa milangoni, wanaomba tuwasaidie namna ya kusoma Chuo Kikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe sana Serikali yangu, tuamue tu kwamba sasa mikopo itakuwa kwa wanafunzi wote wanaoenda Chuo Kikuu mradi tu wamechaguliwa. Kama haiwezekani kuwasomesha watoto wote kwa kuwa wanafunzi ni wengi wanaosoma Chuo Kikuu, basi tuanzishe utaratibu kwamba kama tumeamua division one, division two ndiyo watakaopata mikopo, basi iwe hivyo ili mwanafunzi ajue mapema kwamba mimi nimepata division three au nimepata points ambazo haziruhusu kupata mkopo, basi aanze utaratibu pengine wa kujiunga na vyuo vingine kuliko kuruhusu mtoto anadahiliwa anaenda Chuo Kikuu, anakosa mkopo mwisho wa siku wengine wanajiingiza kwenye tabia ambazo au mienendo ambayo haifai katika nchi yetu. Kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Profesa Ndalichako wakae huko ndani Serikalini washauriane namna gani ya kuwasaidia Watanzania hawa wanaotaka kuendelea na masomo ya elimu ya juu.

Mheshimiwa mwenyekiti, jambo la pili ni juu ya lugha ya kufundishia, tumekuwa in dilemma siku zote, ukiangalia hata sera yenyewe ya elimu unakuta kule ndani kuna contradiction, sehemu moja inafuatana sikumbuki sehemu gani kama siyo 3.2 to nine inasema kwamba elimu ya kufundishia sasa itakuwa Kiswahili, lakini ukienda chini yake pale inasema kwamba elimu tutaendelea na kufundishia maana elimu ya sekondari kwa lugha ya Kiingereza sasa ni vizuri tukaamua, kwa sababu hawa watoto tunawachanganya wanapokuwa shule ya msingi wanasoma Kiswahili, wanapofika form one wanaanza Kiingereza kwa hiyo kwao inakuwa ni lugha ya pili sasa na kitaalam ni kwamba ili mwanafunzi asome vizuri ni vizuri atumie lugha yake ya kwanza. Hiyo Walimu wote tunajua na sisi wote Walimu tunajua kwamba lugha ya kwanza ndiyo inamwezesha mtoto ku-acquire maarifa kivizuri zaidi na aki- acquire vizuri kwa sababu uelewa wake ni mzuri ataendelea vizuri na mwisho wa siku atakuwa na ufaulu mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana ukiangalia matokeo, ukiangalia matokeo ya shule ya msingi, shule ya msingi wanafaulu sana watoto wakifika sekondari wanaanza kufeli. Kwa hiyo ukiangalia wanaoshindwa kuendelea na masomo ya kidato cha tano sekondari ni wengi zaidi ukilinganisha na walioanza pale form one. Ukichunguza ndani lugha ya Kiingereza ni shida Tanzania. Kwahiyo tuamue vizuri, tuamue kwamba tunaamua kufundishia Kiingereza, toka darasa la kwanza ama toka awali mpaka Chuo Kikuu au tunafundisha Kiswahili toka awali mpaka Chuo Kikuu. Kwa hiyo niombe tusibaki na dilemma hii itatusumbua kwa hiyo ni vizuri tukae tuamue kwamba ni lugha gani sasa tunaenda kufundishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni juu ya udhibiti wa ubora. Niipongeze Serikali nipongeze hatua zilizochukua kuhakikisha kwamba zinaanza kujengwa ofisi, lakini pia tunaanza kuwanunulia magari. Tatizo la magari imekuwa ni changamoto kubwa sana ukienda kwenye halmashauri nyingi magari wanayotumia Wadhibiti Ubora yamechoka na siyo magari tu hata mafuta ya kwenda kufanyia ukaguzi hawana utakuta mara nyingi wanaenda kukagua shule binafsi zisizo za Serikali kwa sababu wale wanalipa ada wanatumia zile fedha kwa ajili ya kuwajazia mafuta na posho, lakini shule za Serikali imekuwa tatizo kwa sababu wakati mwingine hawapati posho wanategemea halmashauri yenyewe iweze kuwachangia mafuta ili waweze kukagua na hili ndiyo jicho la Serikali kwenye upande wa elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Wizara ya Elimu iwawezeshe Wakaguzi, Kitengo cha Ukaguzi ili muda wowote wanapoona kuna dalili za mwenendo kwenye shule fulani hauendi vizuri au taaluma haiendi vizuri waweze kwenda kukagua muda wowote ambapo anaweza akafanya hiyo kazi, kuliko wanavyokuwa na bajeti ndogo ya mafuta na magari yenyewe hawana ya kutosha, kwa hiyo inakuwa shida kwenda kukagua mpaka wasubiri wawezeshwe. Kwa hiyo hii sasa inazorotesha ubora wa elimu kwenye shule zetu. Hivyo, nimwombe sana ndugu yangu Profesa Ndalichako, yeye ni mtaalam wa elimu, lakini wote pia ni wataalam awawezeshe hawa Kitengo cha Udhibiti Ubora ili waweze kupata fedha za kutosha kwa ajili ya kuendelea kufanya kazi zao vizuri ili tuweze kuboresha ubora wa elimu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia juu ya elimu ya ufundi, nilishauri mara kadhaa hapa, ni vizuri turudishe ule utaratibu wa zamani kwamba tuwe na shule za misingi za ufundi, kila kata kuwe kuna shule mojawapo ambayo itakuwa na mchepuo wa ufundi, lakini pia kwenye tarafa au kwenye halmashauri tuwe na Sekondari moja ya ufundi ili tuanze kuwazalisha mafundi michundo wengi. Ilivyo sasa hivi, mpaka mtu amalize form four, amefeli ndiyo anaanza kutafuta fursa ya kuajiriwa anakwenda kusoma Chuo cha VETA. Kwa hiyo tukianza huko chini kwanza tutakuwa na mafundi wa kutosha kuanzia shule za misingi, hata kama amemaliza la saba amefeli, hajaendelea na masomo ya sekondari ana uwezo wa kujitegemea kwa sababu ana skills ambazo zitamfanya aweze kujiajiri yeye mwenyewe. Hivyo hivyo anayemaliza form four badala ya kusubiri ajira nyingine anaweza akaanzisha shughuli na mwisho wa hizo shughuli hizo ndogo ndogo zitafanya watu wengi waweze kuajiriwa kwa mfano kwenye useremala, kwenye umakenika mdogo kwenye ufundi uashi na ufundi mwingine, mwingine mwingi tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe Serikali yangu tuanze kuanzisha huo, pamoja na kwamba tunaanzisha vyuo na tunaziboresha hizi Focal Development Colleges, hizi tuziwezeshe ni kweli, lakini pia tuangalie shule za msingi ambazo tunaweza tukaanzisha kwenye kila kata, lakini pia kwenye kila tarafa au halmashauri kuwe na shule ya ufundi na mwisho wa siku tutakuta kwamba tumepata wataalam wa kutosha kuliko ilivyo hivi sasa hivi. Kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Profesa Ndalichako na Mheshimiwa Ole Nasha na wataalam wengine wa Wizara, hebu wajifungie ndani waweze kuangalia namna gani tunaweza tukafanya haya mambo yote yaweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nikushukuru sana kwa nafasi hii na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kushukuru kwa kupewa nafasi ya kuchangia Mpango huu wa mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna anavyotekeleza majukumu yake. Tumeona mipango mizuri na miradi mikubwa inatekelezwa, kwa hiyo, nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimpongeze pia Waziri wa Fedha na Naibu Waziri wake kwa namna wanavyosimamia mapato na hata utekelezaji wa mipango mbalimbali, nawapongeza sana. Taarifa mliyoileta ni nzuri na inaeleweka, tunaiona mipango mnaisimamia vizuri na inatekelezwa vizuri naamini na hii itatekelezwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze kuzungumzia upande wa kilimo hasa uwekezaji katika sekta ya kilimo. Kama taarifa inavyoeleza kwamba sekta ya kilimo ndiyo inayochangia asilimia 28.2 katika pato la Taifa lakini pia inaajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania lakini ukiangalia ukuaji wake ni mdogo sana, bado uko asilimia 5.3. Sekta ambayo inaajiri watu wengi lakini bado ukuaji wake upo asilimia 3. Kwa hiyo, hapa bado tuna kazi kubwa ya kufanya. Niiombe Serikali tujitahidi kuwekeza kwenye kilimo ili tuweze kwanza kupanua ajira, lakini pia fedha za kigeni nyingi sisi kama Tanzania tunategemea sana kwenye mazao haya ya biashara lakini pia kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mazao ya biashara kama chai, kahawa, korosho na mengineyo, yakisimamiwa vizuri toka mwanzoni, kwa maana ya toka kwenye uzalishaji hata kwenye uchakataji na mwisho yakatafutiwa soko zuri yana uwezo wa kuingiza fedha za kigeni nyingi sana. Kuna nchi nyingine uchumi wao unategemea tu mazao kama haya lakini wanafanya vizuri na wanapiga hatua kubwa. Kwa hiyo, niombe sana jambo hili liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kenya ni nchi ya jirani tu haya mazao inayategemea sana, inauza kwa kiasi kikubwa lakini pia bei yake ipo juu ukilinganisha na Tanzania sisi bado tupo chini. Kwa mfano, kwenye zao la chai na kahawa, haya mazao yameyumba sana na ukiangalia hata usimamizi wake siyo mzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Njombe sisi tunalima chai, ukienda Lupembe hivi leo kuna chai inamwagwa yaani maana yake hakuna mnunuzi au wanakosa mnunuzi au mnunuzi hana uwezo wa kuchakata chai yote.

Kwa hiyo, unaweza ukaona namna gani tunavyopoteza fedha za kigeni kupitia hii sekta ya kilimo. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweke usimamizi mzuri kuanzia kwenye uzalishaji, uchakataji na mwisho wa siku na soko lenyewe lisimamiwe vizuri ili tuweze kuongeza uchumi wa Taifa letu na pato kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine linalotatiza kwenye sekta ya kilimo ni miundombinu. Ukiangalia kwenye maeneo ambako uzalishaji ni mkubwa miundombinu ya barabara sio mizuri. Hivyo, usafirishaji wa mazao toka shambani kwenda viwandani na badaye kutoka viwandani kwenda masokoni unachukua muda mrefu na mwisho wa siku kuathiri ubora wa mazao haya na mwishoni unakuta kwamba hata pato lake linaathirika kwa sababu kwenye soko la dunia huwezi kushindana kwa sababu ubora wake unakuwa umepungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kwenye upande wa miundombinu hasa barabara hizi zinazounganisha mkoa mmoja mpaka mkoa mwingine, kwa mfano Njombe pale katikati tunazalisha chai, miti, nguzo, parachichi na mazao mengine lakini shida ni kuunganisha mikoa. Kwa mfano, kwenye Jimbo langu la Lupembe barabara ile ya Kibena – Lupembe – Madeke, pale katikati kuna uzalishaji mkubwa sana, ile barabara ingekuwa ya lami tayari mazao yanayozalishwa maeneo ya Lupembe na maeneo mengine kama Mlimba kule ndani yangeweza kupelekwa sokoni na mwisho wa siku tukapata faida kubwa kupitia mazao haya yanayozalishwa pale lakini kupitia sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali iongeze bajeti TARURA ili barabara zinazoenda vijijini ziweze kujengwa. TARURA wanashughulikia barabara zote zinazoenda kwenye mashamba na kwenye vijiji mbalimbali waongezewe bajeti. Hivi ilivyo sasa hivi bajeti yao ni ndogo, hawawezi kutengeneza barabara zote zinazoenda kwenye mashamba haya kwa sababu hawana fedha. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Dkt. Mpango katika mipango yako ile angalau kipindi hiki tujitahidi kuwaongezea TARURA fedha kwenye bajeti yao ili waweze kukamilisha jukumu zima la kutengeneza barabara kwenye maeneo ya vijijini ambako huko ndiko kuna uzalishaji mkubwa wa mazao haya ya chakula lakini pia mazao haya ya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie pia juu ya Mradi wa Mchuchuma na Liganga. Mradi huu tumekuwa tukiusikia muda mrefu kwamba utatekelezwa. Nipongeze hatua za Serikali kwenye ukurasa wa sita wa taarifa ya Mheshimiwa Waziri lakini pia kwenye kifungu kidogo kile cha (6) inaeleza kwamba kazi ambazo zimeshatekelezwa ni pamoja na utafiti wa kina kuhusu wingi wa madini lakini pia thamani ya madini na aina ya miamba na uhakiki wa mali za wananchi watakaopisha eneo la mradi. Niipongeze sana Serikali kwa hatua ambayo mmefikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa twende mbali zaidi, twende kuhakikisha kwamba tunautengea fedha za kutosha mradi huu ili uweze kuanza kwa kuwa tukianza kuzalisha ule mkaa pale Mchuchuma utaweza kuzalisha umeme wa kutosha na umeme huu unahitajika sana. Pamoja na kwamba tunampongeza sana Rais tumeanza kukamilisha ule Mradi wa Rufiji, ni kweli ni mradi mkubwa, lakini huu mradi unategemea hali ya hewa, hali ya hewa ikibadilika tunaweza ukapata shida pia, uzalishaji wa umeme wa Rufiji unaweza ukapungua lakini kumbe tukiwa na mradi mwingine wa Mchuchuma ule unaozalisha umeme kwa kupitia makaa ya mawe haya maeneo mawili yanaweza yakasaidiana kuhakikisha kwamba viwanda vyetu na shughuli za kiuchumi katika nchi yetu zinaendelea vizuri bila kuathirika. Kwa hiyo, tusitegemee source moja, tuwe na source zote mbili. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mpango tuongeze fedha kwenye mradi huu ili uanze kutekelezwa na hatimaye umeme uanze kuzalishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia taarifa inaeleza kwamba kuna madini mengine pia yatazalishwa, kwa mfano kuna vanadium, titanium pamoja na chuma. Hizi vanadium na titanium zinatumika sana kwenye kujenga engine za magari lakini pia titanium inatumika kujenga engine za ndege, ni mradi muhimu sana. Kwa hiyo, kumbe badala ya kuagiza baadhi ya malighafi kutoka nje kwa ajili ya ujenzi wa engine tutaweza kupata malighafi hapahapa nchini. Kwa hiyo, tunaweza tukauza lakini pia tukazitumia sisi kama nchi kwa ajili ya kutengeneza engine hizi za ndege hapahapa za mwendokasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ni juu ya elimu. Kuna shida kubwa sana kwenye upende wa walimu hasa wa shule za misingi. Shule nyingi zina uhaba wa walimu wa shule za misingi. Kwa hiyo, niombe katika Mpango wetu tujikite kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi ya walimu watakaoajiriwa wa shule za msingi ili wasaidie kutoa elimu bora kwenye shule hizo. Pia walimu wa sekondari kwenye shule zetu bado ni wachache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri katika mipango yetu tujitahidi kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi ya watakaokuwa wanaajiriwa kwenye shule za msingi ili watoto wetu waweze kupata elimu bora. Maana watoto kama wataenda bila walimu au walimu wanafundisha darasa kubwa la watu 100 au 80 watoto uelewa wao utakuwa ni mdogo, kuna wengine hawataelewa vizuri. Kwa hiyo, tujitahidi kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi ya walimu hasa shule za msingi na sekondari ili watoto wetu waweze kupata elimu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni juu ya ndege. Tumeshanunua ndege za kutosha na tunaendelea kununua, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada zake za kununua ndege lakini bado sijaona sehemu ambayo inaelezea utaratibu wa kuongeza mafundi wa ndege. Ni kweli tumenunua ndege, je, hizi ndege tutakuwa tunaenda kutengeneza nje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali ianzishe utaratibu wa kuwa na kitengo na mafunzo maalum kwa ajili ya ma-engineer watengenezaji wa ndege ili ndege zetu baadaye tusitegemee kwenda kutengenezwa nje ya nchi, ziweze kutengenezwa hapahapa nchini. Kwa hiyo, tuanze utaratibu kama ni kuwapeleka nje kwa sababu tayari tumeshanunua Bombardier tuwapeleke huko kwenye viwanda hivyo vinavyozalisha hizo ndege na kwenye vyuo hivyo vya kutengenezea hizo ndege ili waweze kujifunza na tuwe na wataalam wetu ambao watakuwa ni mafundi wa ndege zetu. Itakuwa siyo vizuri ndege inaharibika inabidi ulete mtaalam kutoka nje au ulete fundi kutoka Marekani lakini tukiwa na mafundi wetu kwanza tutapunguza gharama za kukodi mafundi hawa lakini pia tutaongeza ujuzi na ajira kwa vijana wetu ambao wapo hapahapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nipongeze sana Serikali kwa juhudi zake za kuhakikisha kwamba inajitahidi kuboresha huduma ya usafirishaji kwa kupitia reli, hasa hii reli ya Standard Gauge. Nampongeza Waziri anaeleza kwenye taarifa yake kwamba reli ya TAZARA itaenda kuboreshwa lakini mmeanza kwanza kununua vichwa vipya saba vya treni na mitambo mbalimbali. Ni muhimu reli ile ikaboreshwa kwa sababu ukanda wa Kusini mizigo mizito yote inapita kwenye barabara lakini tukiwa na reli hizi Nyanda za Juu Kusini na nchi ya Zambia tutaweza kusafirisha mizigo mizito kwa kupitia reli hii na hatimaye barabara zetu zinazoenda Mbeya, Ruvuma na Zambia zitadumu muda mrefu kwa sababu mizigo mingi mizito sana itasafiri kupitia reli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa nafasi. Naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema, lakini nashukuru pia kwa kupata nafasi ya kuchangia kwenye hizi taarifa zote za hizi Wizara. Nianze kuwapongeza sana Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati za Wizara zote, Wizara ya TAMISEMI, Katiba na Sheria lakini pia na Sheria Ndogo kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya na wakaleta taarifa nzuri ambayo wametusomea hapa wametuletea hapa, nawapongeza sana. Pongezi kwa namna ya pekee Mawaziri wa Wizara hizi zote mbili, hasa nikianza na Waziri wa TAMISEMI na Manaibu Waziri wote wawili na watendaji wake wote, lakini pia na Watendaji wa Wizara nyingine na Mawaziri wa Wizara hizi zote nyingine ambazo taarifa zao zimewasilishwa hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia kwenye upande wa TARURA, Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini. Kama ilivyoelezwa kwenye taarifa imeoneshwa vizuri sana kwamba TARURA wanashughulikia barabara zenye urefu wa kilometa 108,946. Hizi ni barabara nyingi sana, na hizi barabara ni zile ambazo zimesajiliwa lakini bado kuna barabara nyingi ambazo hazijasajiliwa, nazo pia kwa namna moja au nyingine pengine wanashughulikia nazo, lakini ukiangalia kwenye bajeti yetu bado TARURA wanapewa fedha kidogo sana kama walivyoeleza wenzangu. Sasahivi wanapewa kwenye bajeti asilimia 30 na asilimia 70 inaenda kwa TANROAD, mimi, kama walivyosema wenzangu, nilikuwa napenda nipendekeze kwamba angalau wangeweza kuongezewa ikafika asilimia 45 hivi ili barabara nyingi hizi zinazoenda huku Vijijini ambako ndiko asilimia 80 ya wananchi wanashughulika na kilimo, ili waweze kusafirisha mazao yao vizuri ni lazima barabara za huko ziwe nzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kupitia barabara hizo barabara tutaweza kukuza uchumi wetu; na ukiangalia mapato mengi halmashauri nyingi hasa za Vijijini zinategemea sana hizi barabara. Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa kwamba kuna baadhi ya halmashauri hazilipi Madiwani, ni kwa sababu tu hawapati mapato ya kutosha na inawezekana kinachochangiwa wasipate mapato ya kutosha ni kutokana na kwamba barabara ikifika misimu ya mvua kama hii sasahivi mizigo haiwezi kusafiri. Kwa hiyo maana yake mapato yale ambayo wanatakiwa kukusanya kupitia hizi barabara hawawezi kuyapata; kwa hiyo na hatimaye shughuli nyingi za maendeleo, lakini shughuli nyingi pia za halmashauri zinakwama kwa sababu barabara hizi hazipitiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua mfano kwangu mimi kwenye Jimbo langu mimi kwenye Jimbo langu Jimbo la Lupembe asilimia 80 ya mapato linategemea hizi barabara za vijijini, na miezi kama hii ambapo mvua zinanyesha nyingi barabara hizi zote hazipitiki. Kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri mkikaa kwenye Baraza lenu mpitishe hili kwamba angalau TARUARA wapewe hela za kutosha. Wakipata asilimia zaidi ya 40 hivi itakuwa nzuri na barabara nyingi zitaweza kuboreshwa na hatimaye uchumi wa halmashauri utakuwa na mapato yataongezeka na hatima yake miradi mingi ya maendeleo itatekelezwa kwa sababu vyanzo vya mapato vinaweza kupatikana kirahisi, pia mizigo inaweza kusafiri kirahisi kutoka vijijini kwenda mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichangie kuhusu mpango wa kurasimisha, biashara na rasilimali mbalimbali ikiwemo ardhi, nyumba na biashara. Mimi niongelee kidogo juu ya upande wa ardhi na makazi. Tunaushukuru sana, Serikali kwa kuanzisha mpango huu, na unaendelea vizuri na tunaona ardhi zinarasimishwa zinakuwa na thamani. Ilivyokuwa kabla ya mpango huu ardhi nyingi maeneo mengi ilikuwa haina thamani kwa sababu zilikuwa hazijarasimishwa; lakini pia na makazi tunajua watu wengi wamejenga kwenye viwanja ambavyo hazijapimwa, lakini Serikali imeendelea kurasimisha kupitia MKURABITA ili ardhi hizi au nyumba hizo ziweze kutambulika na hatimaye ziweze kupata hati. Lakini tuna changamoto kubwa sana changamoto ya Maafisa Ardhi, pia na Maafisa Mipango Miji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya halmashauri hususan halmashauri za vijijini nyingi hazina wataalam wa ardhi, hazina Maafisa Ardhi Wateule na Maafisa Mipango Miji. Halmashauri ya kwangu, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe nayo ni miongoni mwa halmashauri ambayo muda mrefu haina Afisa Ardhi Mteule na pia haina mtaalam wa mipango miji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunashindwa hata kupanga mipango ya ardhi, tunashindwa hata kupima na kutoa hati imekuwa ni vigumu kwa sababu hatuna wataalam. Kwa hiyo tuombe sana, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo tusaidie tuweze kupata Afisa Mteule pamoja na mtaalam wa mipango miji ili nasi tuweze kupata wataalam ambao watatusaidia kutoa hati pamoja na kurasimisha ardhi na makazi. Vilevile tuweze kupanga miji ili tuweze kupata vyanzo vingine vya mapato na wakati huo huo miji yetu iweze kukaa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu kukamilisha maboma. Tunashukuru sana Serikali imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma kama vile majengo ya afya na majengo ya elimu. Kwenye halmashauri yetu sisi bahati mbaya hatukupata pesa ya upande wa afya, kwa maana ya vituo vya afya, lakini niishukuru sana Wizara ya TAMISEMI mmetupatia milioni 200 kwa ajili kujenga kituo cha afya kimoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kupitia Wizara yako Mheshimiwa Waziri mtusaidie tuweze kuongezewa fedha, tukipata angalau milioni 400 tuweze kukamilisha hicho kituo cha afya, na ikiwezekana mtupatie tupate vituo viwili kama zilivyo halmashauri lingine ambazo zimepata sisi tulikosa tumepata mwishoni hizo milioni 200; basi mtuongezee tuweze kukamilisha ujenzi wa vituo vyetu vya afya na maboma mengine ambayo yapo kwenye Halmashauri yetu ya Wilaya ya Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwahiyo naamini kwamba tukifanya hivyo tutakuwa tumeboresha sana na watu wengi watapata hii huduma ya afya kirahisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna changamoto kubwa pia katika uboreshaji wa hivi vituo vya afya na kwenye upande wa elimu. Sasahivi tuna changamoto kubwa ya wataalam, wahudumu wa afya na walimu, hasa walimu wa shule za msingi kwenye elimu. Niombe sana Wizara iajiri walimu wa kutosha ili tuweze kuhakikisha kwamba shule zetu zinapelekewa walimu wa shule za msingi. Kuna baadhi ya shule zina walimu watatu na nyingine zina walimu wanne; kwa hiyo hili ni tatizo kubwa. Hatuwezi kutegemea kuwe na ubora wa elimu kama walimu wanaofundisha ni wanne. Kuna shule ambayo nilisoma mimi Mheshimiwa Waziri inaitwa Shule ya Msingi Kanikelele ina walimu sita tu na wanafunzi wako mia saba na kitu leo hii.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana, tukiongeza ajira za walimu tutasaidia halmashauri nyingi ziweze kupata walimu na hatimaye watoto wetu waweze kupata elimu bora. Kwa hiyo ilivyo sasahivi watoto wengi wanashindwa kupata elimu bora kwa sababu walimu mashuleni hawapo. Kwa hiyo niombe sana katika mpango wetu katika bajeti hii tujikite kabisa kuajiri walimu, lakini pia tujikite kuajiri wataalam wa afya ili vituo vyetu vya afya ambavyo tumevianzisha viweze kupata watalam, pia na shule zetu hizi ziweze kupata walimu ili watoto wetu waweze kusoma vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nililotaka nichangie kidogo juu ya mikopo ya walemavu; wenzangu wameeleza pia; lakini niseme kwamba kwenye upande wa hasa ile asilimia mbili; niombe, kuna wale walemavu ambao wao wenyewe hawana, mmoja amesema hapa kuhusu wale wenye utindio wa ubongo au wengine wana ulemavu ambao hauwawezeshi hata kufanya shughuli yoyote; tuwapatie basi wazazi wao ili waweze kuingizwa kwenye kikundi ili nao wahesabike na ili waweze kupata hii mikopo. Hii ni kwa sababu ilivyo sasahivi inataka mlemavu mwenyewe aweze kuwepo kwenye kundi. hii itawatenga baadhi ya walemavu watashindwa kupata mikopo kwa sababu hawatakuwa na uwezo wa kuingia kwenye kundi. Sasa tukitumia wazazi ama walezi wao wataweza kunufaika na hiyo mikopo ambayo inatolewa na halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa nafasi na naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kidogo kwenye hii bajeti ya mapato na matumizi. Nianze kuanza kwa kukushukuru wewe binafsi na kukupongeza kwa kuendelea kukalia hicho Kiti, usiwe na wasiwasi wewe tulia kama jina lako linavyosema, sisi tuko pamoja na wewe kuhakikisha kwamba mambo yanaenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee nimpongeze Waziri wa Fedha na Naibu Waziri wake kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Bajeti yao iliyoletwa inaonyesha weledi na umahiri mkubwa wa kazi ambayo wamepewa na Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, inaonyesha kazi hii wanaweza wakaimudu vizuri na watatusaidia kuhakikisha kwamba uchumi wetu unakua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuchangia kidogo kwenye upande wa huduma ya maji. Tumesikia Wabunge wengi wamesema sana hapa kuhusu suala la maji na wametoa mapendekezo mengi sana, tunaomba jambo hili tulitilie mkazo sana na tulifanyie kazi. Wabunge wapendekeza kwamba tuwe na tozo ya Sh.50 ili kwenye shilingi bilioni 125 basi ziongezeke zifikie shilingi bilioni 250 ili wananchi wetu wengi ambao wanaishi huko vijijini waweze kupata maji, tatizo liko wapi? Kama sisi ndiyo tunaopanga na tunawashauri kwa nini tusiongeze hizi Sh.50 kwa lita ya mafuta ili wananchi wengi wanaoishi vijijini waweze kupata maji? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vijijini kule sasa hivi tunawahamasisha wajenge vyoo vya kisasa lakini vijiji vingi havina maji. Hata ukiangalia kwenye bajeti ya maji, miradi mingi ya maji mikubwa mikubwa imeelekezwa mijini na hata fedha iliyotengwa kwa maana ya maji vijijini bado zinaelekezwa mijini. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa majumuisho tunataka kujua ni nini amefanya hasa kuhakikisha tozo ya Sh.50 kwa kila lita moja ya mafuta inaongezeka na kuwa Sh.100 na hatimaye tuweze kuongeza usambazaji wa maji vijijini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kidogo kwenye kilimo, niipongeze Serikali kwa kuondoa kodi hasa kwenye mazao ya matunda na mboga mboga kwa maana ya mazao yale ambayo hayajafanyiwa processing, niwapongeze sana. Pia niipongeze Serikali kwa kupunguza kodi kwa baadhi ya mazao ya biashara kama vile chai, kahawa, korosho na mazao mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba pamoja na kupunguza kodi kidogo bado tusipokuwa makini tutafanya Watanzania wabaki kwa kutokuwa na uwezo wa kulima kwa kiasi kikubwa na kuweza kuzalisha kiasi ambacho kitatutosha kulisha hivi viwanda vyetu ambavyo tunaanza. Ni lazima tuhakikishe kwamba hawa wananchi wanawezeshwa ili kuzalisha kwa kiasi cha kutosha, kingi zaidi na kuzalisha matunda ambayo yanakuwa ni bora ili yaweze kupata soko, waweze kupata kuuza kwenye hivi viwanda ambavyo tunatarajia vitakuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutawezaje kufanya hivyo? Ni lazima tuwawezeshe kwa kuwapelekea Maafisa Ugani. Vijiji vingi sasa hivi havina Maafisa Ugani, wananchi wanalima kilimo kile kile cha utamaduni bila kuzingatia kanuni bora za kilimo. Kwa hiyo, tuombe Wizara husika kwa pamoja tupeleke Maafisa Ugani wa kutosha ili waboreshe kilimo vijijini na hatimaye waweze kupata faida kwenye mazao yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nijaribu kuchangia kwenye upande wa elimu. Ni kweli Serikali imepeleka fedha nyingi, tumeona ina mpango wa kupeleka trilioni 4.77 ambayo ni sawasawa na asilimia 22.1. Fedha hizi ili ziweze kufanya kazi ambayo imekusudiwa. Ni muhimu sana hizi fedha zipelekwe kwenye maeneo haya ya shule kwa wakati. La sivyo fedha hizi hazitafanya yale malengo ambayo yamekusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumejifunza miaka ya nyuma, fedha zimekuwa zikitengwa kwa ajili ya kuendeshea mashule, lakini zinakwenda kwa kuchelewa, zinaenda miezi ya Tano na Sita; na inapofika tarehe 30 wale Wakurugenzi na Wakuu wa Shule wanatakiwa kurejesha hizi fedha tena Hazina, zinarudi tena bila kufanya kazi. Kwa hiyo, niombe mamlaka husika zipeleke hizi fedha kwa wakati ili zifanye kazi ambazo zimekusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, niongee kidogo pia kwenye suala la afya. Ni kweli, nitoe pongezi kwa Serikali, tumetenga trilioni 1.99 ambayo ni sawasawa na asilimia 9.2 ya bajeti nzima na hizo fedha tumesema zinaenda kwa ajili ya vifaa tiba, vitendanishi (reagents) na miundombinu, kwa hiyo, tuombe hizi fedha ziende kwenye vituo vya afya vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wengi wanategemea sana hivi vituo vya afya, kwa hiyo ni muhimu sana kuviboresha ili kuhakikisha kwamba angalau vituo vyote vya afya vinatoa huduma ya upasuaji pamoja na huduma kwa akinamama. Tunasema wanawake na watoto wengi wanafariki, ni kwa sababu huduma za afya hasa vijijini hazijaboreshwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia statistics wanaokufa wengi ni wale watu wa vijijini, ni kwa sababu wanakwenda hospitalini kwanza kwa kuchelewa kutokana na kutembea umbali mrefu, wakifika hakuna huduma nzuri, wanatakiwa wasafiri au wasafirishwe kwenda kwenye Hospitali za Wilaya ambazo zipo mbali. Wanafika huko wakiwa wamechelewa, hatimaye watoto wao wanafariki au wanapata operation na mwisho wa siku wanapata matatizo mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nisemee kidogo kuhusu hii sheria ya magari, kwa maana ya kodi ya usafiri na uhamisho wa umiliki, ambayo ipo Sura namba 124, hasa kwenye upande wa pikipiki. Katika Ilani yetu tulisema tunataka hawa bodaboda sasa kwa hizi kazi wanazozifanya za kusafirisha, ziwe ni kazi rasmi. Nilitegemea kwamba leo hii tungekuwa tunaongelea kupunguza kodi za pikipiki, kwa kuwa hizi pikipiki nyingi wanazozitumia ni zile ambazo wamekodishwa na matajiri. Sasa tunataka hawa waendesha bodaboda waendelee kubaki maskini? Waendelee kuwasaidia watu wengine wenye fedha?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaomba hili ongezeko la kodi kutoka sh. 45/= mpaka 95/= liondolewe ibaki ile ile na ikiwezekana ipunguzwe zaidi ili vijana wetu ambao huko nyuma walikuwa wanafanya kazi za wizi, utapeli na kupiga watu nondo wajiajiri kwenye uendeshaji wa boda boda. Kwa kuwa boda boda zimesaidia kutafuta ajira kwa hawa vijana wetu, basi tupunguze kodi za pikipiki ili nao waweze kununua pikipiki na hatimaye wakapata fedha kwa ajili ya kuendeshea familia zao na maisha yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wamesema pia juu ya kodi ya mitumba. Hakuna mtu ambaye hatambui, wote hapa ni Watanzania na wengi wetu tunatoka vijijini, wananchi wengi wanaoishi vijijini ndizo nguo wanazozitegemea. Mwananchi wa kijijini hutegemei akaenda kununua nguo dukani, anategemea mwisho wa mwezi aende kwenye mitumba apate nguo za kuweza kujisitiri, sasa sisi tunaongeza kodi. Ni vizuri tufanye kwanza utafiti, au wakati huu ambao tunataka kupeleka viwanda vya uzalishaji wa nguo basi kodi ziwe za chini, ili wananchi wengi waishio vijijini waweze kumudu kununua nguo. La sivyo wananchi wetu vijijini watashindwa kununua hata nguo tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa uamuzi wa kutoa elimu bure toka shule ya msingi mpaka kidato cha nne. Hii imesaidia kuongezeka kwa udahili wa wanafunzi wa darasa la kwanza na kidato cha kwanza. Ufaulu wa watahiniwa wa darasa la saba na wale wa kidato cha sita unaendelea kupanda wakati ngazi ya chini, yaani sekondari, umeshuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hapa ni Walimu. Walimu wa masomo ya sayansi ni wachache sana. Kuna baadhi ya shule hazina kabisa Walimu wa masomo ya Hisabati, Fizikia, Biolojia na Kemia. Shule ambazo hazina Walimu wa masomo haya bado ufaulu wa wanafunzi katika mitihani ya kidato cha nne ni mbaya sana. Hivyo, ni muhimu katika mipango ya Serikali tuwekeze vya kutosha katika kuzalisha Walimu wa masomo ya sayansi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nyumba za Walimu katika shule nyingi zimekuwa chache sana. Walimu wengi bado wanakaa mbali na shule, kuna baadhi wanatembea umbali wa kilometa tano mpaka saba kwenda shuleni, hasa maeneo ya vijijini; hivyo, hufika shuleni wakiwa wamechoka na wakati mwingine kushindwa kutekeleza majukumu yao ya kuwasaidia wanafunzi. Serikali iweke utaratibu madhubuti wa kujenga nyumba za Walimu, hasa kwa shule zilizopo vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa hatua inayochukua ya kuanzisha Vyuo vya Ufundi (VETA) kwenye baadhi ya maeneo. Kwa kuwa, tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, hasa viwanda vya kati, tuhitaji zaidi mafundi mchundo ambao ndio watafanya kwenye viwanda hivi. Hivyo ni muhimu kuweka utaratibu wa kujenga vyuo hivi kwa kila Wilaya. Kuendelea kuongeza Vyuo Vikuu haitusaidii sana kutatua tatizo la ajira na nguvukazi, kwani wahitimu wa Vyuo Vikuu ni Maafisa ambao wanatarajiwa kwenda kusimamia kazi katika sekta mbalimbali. Je, ni nani atafanya kazi katika viwanda hivi kama hatuna watu hawa wenye elimu ya kati?
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada za Serikali katika kuendelea kutoa mikopo kwa wanafunzi wa Elimu ya Juu, bado vijana wengi wamekuwa wakikosa mikopo hiyo. Vijana wengi, hususan watoto wa maskini wanaotokea vijijini ndio ambao wamekuwa wakikosa mikopo. Serikali ipitie upya vigezo vinavyotumika katika utoaji wa mikopo. Vigezo hivyo viwe wazi na ikiwezekana Wakuu wa Shule za Sekondari wapewe hayo maelekezo ya jinsi Bodi ya Mikopo inavyotoa tathmini ya kukopesha wanufaika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iwe na utaratibu wa kufanya projection/forecast mapema ili kujipanga na kujua mahitaji ya kiasi cha fedha kitakachohitajika kwa mwaka husika ili tuingize kwenye bajeti ya Serikali. Hii inaweza kufanyika kwa kujua ni vijana wangapi watahitimu kidato cha sita kwa mwaka huo wa fedha? Tunatarajia watafaulu wangapi? Hii itatusaidia kupunguza baadhi usumbufu na matatizo yanayowapata kwa kukosa mikopo hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Naipongeza Serikali kwa kuweka mpango wa kuendeleza utafiti katika kilimo kwa mazao mbalimbali. Serikali sasa ijikite kwenye utafiti wa masoko ya mazao haya. Wakulima wetu, hususan vijijini, wamekuwa wakijituma katika kuzalisha mazao mbalimbali. Tatizo kubwa limekuwa ni kupata soko la mazao hayo. Kuna baadhi ya maeneo, mfano, Lupembe; mazao ya matunda kama vile nanasi, maembe, parachichi, yamekuwa yakiozea shambani kwa kukosa soko la uhakika. Pia, barabara mbovu au zisizopitika wakati wa kifuku zimekuwa zikiathiri soko la mazao haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri Serikali ikaweka utaratibu wa kutengeneza barabara zinazoenda kwenye maeneo ya uzalishaji ili kuokoa mamilioni ya fedha yanayopotea au hasara wanayopata wakulima kutokana na ubovu wa barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nampongeza Waziri wa Fedha na Watendaji waliopo chini ya Wizara hii kwa kuunda mpango huu. Naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali kwa maana ya Rais mwenyewe, Baraza la Mawaziri na watendaji wote wa Serikali kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya ya kuiweka nchi yetu vizuri ili watu wakae sawa na mwisho wa siku wananchi wapate usawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyosema wenzangu, nianze kuipongeza Kamati yangu kwani nami nipo kwenye Kamati ya Katiba na Sheria, kwa kazi kubwa ambazo tumezifanya kwa ushirikiano wa pamoja. Pamoja na pongezi hizo, kama walivyosema wenzangu, changamoto za Kamati zipo na zimetusababishia pengine tusiweze kutekeleza majukumu yetu vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya changamoto kubwa ambayo tumekumbana nayo ni Kamati kutokuwa na fedha za kutosha hasa fedha kwa ajili ya ziara. Kama walivyosema wenzangu, kiasi kilichotengwa ni kidogo mno hivyo kimetusababishia kukwamishwa katika kutekeleza majukumu yetu. Kamati inapopewa fedha ya ziara inaiwezesha kwenda kujifunza juu ya majukumu yake. Kwa hiyo, Kamati inapokuwa haipati fedha za kutosha inashindwa kutekeleza majukumu yake vizuri ya kuisaidia na kuisimamia Serikali.
Mheshimwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika bajeti zinazokuja tuombe Serikali iweze kutoa fedha za kutosha tukizingatia kwamba Kamati ya Katiba na Sheria ni Kamati ambayo inasaidia wananchi wake kupata haki. Kwa hiyo, tusipojifunza kwa nchi nyingine au kwa wengine wanafanyaje shughuli zao inakuwa ni vigumu kutunga sheria ambayo itakuwa inatenda haki. Kwa hiyo, tuombe awamu inayokuja angalau Kamati zipate fedha za kutosha kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake hasa ya kuisimamia Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ziara zinatuwezesha sisi Wabunge kuweza kujua fedha zilizopelekwa kwenye taasisi mbalimbali kama zimefanya kazi ile ambayo imekusudiwa. Kwa hiyo, inatusaidia kujua value for money. Sasa Kamati inaposhindwa kwenda kwenye eneo husika kwa maana ya site na inapewa taarifa kwenye makaratasi tu lakini haiwezi kuona kitu kilichotendeka kwa uhalisia basi ile value for money hatuwezi kuiona vizuri. Kwa hiyo, niiombe Serikali yetu katika bajeti inayokuja ijitahidi kuhakikisha kwamba inatoa fedha za kutosha kwa ajili ya kufanya ziara ili Wabunge waweze kwenda ziara na kukagua miradi mbalimbali ambayo tumeitengea fedha ili kuona ilivyotekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine linahusu OC kwenye Halmashauri zetu. Halmashauri zimekuwa hazipelekewi fedha za kutosha kwa maana ya OC na hivyo kushindwa kutekeleza majukumu yake. Kwa mfano, Kitengo cha Ukaguzi, siku hizi tunasema Udhibiti Ubora wa Elimu. Kitengo hiki kimeshindwa kufanya kazi yake kabisa, shule nyingi zimeshindwa kufikiwa na wameshindwa kwenda kukagua kutokana na kukosa fedha hasa kwa ajili ya mafuta ya kuendea kwenye maeneo hayo. Hii ni hatari kama tunakuwa na shule ambazo hazikaguliwi. Kuna shule nyingine utakuta miaka mitatu au mitano imepita hazijakaguliwa. Labda ukaguzi unaofanyika ni ukaguzi ule wa muda mfupi wa kuangalia mambo machache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji shule zetu ziweze kukaguliwa, Walimu waweze kupitiwa ili wakaguzi waweze kuwashauri juu ya mbinu za kujifunzia na kufundishia. Tusipofanya hivyo, itakuwa ni vigumu kuwaweka Walimu katika wakati wa kisasa na kuweza kuenenda kadri inavyopaswa kufundisha kulingana na syllabus na mambo ya taaluma yanavyobadilika. Kwa hiyo, ni muhimu hizi Halmashauri zipewe OC za kutosha ili taasisi zote zinazosimamiwa na Halmashauri kwa maana ya Ukaguzi na sekta nyingine ziweze kutekeleza majukumu yake vizuri na hatimaye tutaweza kupata elimu bora na tutaweza kuwa na watendaji wazuri kwa kuwa wana OC ambazo zitawawezesha kwenda kutekeleza majukumu yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nipongeze (kama walivyopongeza wenzangu) juu ya Mfuko wa TASAF, TASAF amekuwa mkombozi wa wanyonge. Huko vijijini sisi Wabunge tunaopita huko tumeona jinsi maisha ya watu yanavyobadilika na kuna maeneo mengine tumeshahamasisha hao wananchi ambao walikuwa wana kipato cha chini waweze kuanzisha miradi midogo midogo ili waweze kujikimu katika maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaiomba Serikali pindi itakapopata hela za kutosha iendelee kuongeza fedha za TASAF ili wananchi wengi maskini waweze kunufaika na fedha hizi kwa ajili ya kujikwamua katika maisha yao na hatimaye kuendelea kuanzisha miradi midogo midogo ambayo hiyo itawaondoa kutoka kwenye umaskini na hatimaye kuwa na hali nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye TASAF pia kuna tatizo limejitokeza kama wenzangu walivyosema, kuna baadhi ya wananchi walifanyiwa tathmini na wakaonekana kwamba wao ni kaya zile za hohe hahe (kaya maskini) na wakaingizwa kwenye mpango wa kupewa fedha lakini baadaye maafisa wetu wamepita na kusema kwamba hizo kaya hazina sifa za kuendelea kunufaika na mfuko wa TASAF. Baadhi ya kaya zilizo nyingi, kuna hizo kaya za wazee ambao hawana uwezo na kuna kaya nyingine wameondolewa kwenye mpango, uwezo wao ni mdogo, wanashindwa kusomesha watoto wao shule na hatimaye kuleta usumbufu na matatizo makubwa. Wengine wametoroka nyumba zao wakihofia kwamba watakamatwa na Serikali kwa kuwa maafisa waliokuwa wanaenda huko wanawatishia kwamba wasiporudisha hizo fedha basi watafungwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyojua Watanzania wanaogopa kufungwa, kwa hiyo wamekuwa wakiacha nyumba wakikimbia kuogopa kushikwa na mkono wa sheria kwa maana ya kurudisha fedha hizi. Tuombe basi Serikali ijaribu kuliangalia jambo hili, kama kweli ni kaya maskini, naomba tujaribu kuwaachia waendelee kunufaika na fedha hizi ili hatimaye waweze kusaidia familia zao kuweza kupata mahitaji muhimu hasa mahitaji ya kujikimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni juu ya uhamisho wa watumishi wa Serikali. Tulikuwa na zoezi la uhakiki, natumaini kwamba Serikali sasa imeshahakiki watumishi, imeshajua nani ni mtumishi hewa, nani ni mtumishi ambaye hana sifa za kuendelea kufanya kazi katika Serikali. Sasa kwa kuwa uhakiki umekwisha basi turuhusu hao watumishi wetu waweze kupata uhamisho. Sasa hivi kuna Walimu wengi wanaomba uhamisho wanakataliwa, kuna watumishi wa sekta ya afya wanakataliwa uhamisho kwa kisingizio kwamba bado tunafanya uhakiki wa watumishi hewa. Tuombe Serikali iweze kufungua milango hasa ya uhamisho ili watumishi wetu waweze kuhama. Kwa sababu ilivyo sasa hivi tukiwaacha hawa watumishi waendelee kuishi huko walipopangiwa kazi wasipate uhamisho ni hatari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vijana wameoa, kuna mabinti wameolewa wanataka kwenda kwa wenzao, lakini wanazuiwa kwa sababu ya kisingizio cha uhakiki wa watumishi. Kwa hiyo, tuombe kwa kuwa Serikali yetu ina mpango na inadhibiti maambukizi ya UKIMWI, tukiwaacha hawa vijana huko ambao wameoa na kuolewa baadaye tutakuta tumewapoteza kwa kujiingiza kwenye vitendo ambavyo vitawapelekea kupata UKIMWI kwa sababu ya kukaa na wenza wao mbali. Kwa hiyo, niombe Serikali yangu iweze kufungua milango ya uhamisho ili vijana wetu waweze kuhama na waweze kwenda waliko wenzi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nilizungumzie na wenzangu wamelizungumzia ni juu ya semina za viongozi. Semina hizi ni muhimu hasa kwa hawa wanaoteuliwa, Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa. Kwa hiyo, tuombe wapewe semina za kutosha ili waweze kuongoza vizuri. Naamini kwamba wametoka kwenye kazi mbalimbali na kama walivyosema wenzangu kuna wengine hawaifahamu vizuri kazi ya Ukuu wa Wilaya na wengine Wakuu wa Idara, tuwape mafunzo ili waweze kusimamia vizuri majukumu yao na wasiwabughudhi watu. Kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge kwamba kuna baadhi ya maeneo wamekuwa wakiwatishia wananchi na watumishi…
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa hii nafasi. Kwa namna ya pekee naomba nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi anazofanya hasa za kuiongoza nchi yetu Tanzania. Niwashukuru Mawaziri wote kwa namna ya pekee nimshukuru Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anazozifanya na Mheshimiwa Jenister Mhagama na Naibu Waziri wake kwa kazi kubwa wanazofanya usiku na mchana kuhakikisha kwamba Watanzania tunapata maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa walioifanya kwa kuimarisha viashiria vya kukua kwa uchumi, hasa kwenye upande wa ujenzi wa barabara. Lengo la Serikali ilikuwa ni kujenga na kukarabati barabara kilomita 692, lakini tumefanikiwa kukarabati na kujenga barabara kilomita 430 ambayo ni sawa na asilimia 62. Naipongeza sana Serikali yangu inayosimamiwa na John Pombe Magufuli na inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongee kidogo kidogo juu ya barabara yetu, hasa barabara yetu ya Lupembe. Barabara ya Kibena, Lupembe, Madeke ni miongoni mwa barabara zilizopangwa kutengenezwa kwa kiwango cha lami, mwaka jana kwenye Bunge la Bajeti tulipitisha shilingi bilioni nane kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami, mpaka sasa bado tenda ya ujenzi wa barabara hii haijatangazwa, nimwombe Waziri mwenye dhamana na Waziri Mkuu mwenyewe aliona ile barabara jinsi ilivyo angalau tuweze kutangaza tender na ianze kujengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni muhimu sana, ile barabara ya Lupembe kwanza inatuunganisha watu wa Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Morogoro kupitia Jimbo la Mlimba. Barabara hii imekuwa ni barabara muhimu ambayo wananchi wetu wa Lupembe wanasafirisha mazao yao. Lupembe tunalima chai, Lupembe tunazalisha mbao, tunazalisha nguzo za umeme, tunazalisha maharage, mahindi, viazi na kila aina ya matunda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyoongea barabara ile kutokana na mvua zinazoendelea sasa hivi haipitiki tena, imekuwa-blocked, kuna eneo kubwa gari zimekuwa zikikwama na hivyo wananchi kupoteza uchumi mkubwa sana kwa mazao yao kuozea barabarani kwa kutoweza kusafirisha au kupitisha kupitia ile njia, kwa mtindo huo maana yake tunakwamisha uchumi wa wananchi wa Lupembe. Naiomba Serikali yangu sikivu itenge hizi fedha ili tuweze kupata uchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyojua Mkoa wetu wa Njombe ni moja ya mikoa ambayo tunaitegemea sana katika uzalishaji wa mazao ya chakula, pia nguzo kama nilivyosema na zao hili la chai. Sasa kama tutakuwa bado hatuna barabara nzuri, itakuwa ni vigumu wananchi
wanazalisha kwa wingi, lakini hawatoweza kuuza au mazao haya hayataweza kufikia soko kwa sababu barabara yetu siyo nzuri na haipitiki wakati wa kifuku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba atakavyokuja kusimama baadaye niweze kujua ni lini sasa Serikali itatangaza tender ili barabara hii ianze kujengwa kwa kiwango cha lami kadri ilivyokuwa tumekubaliana katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi pia katika bajeti ya mwaka jana, kwa hizo fedha tulizotenga bilioni nane.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa kilimo, Mkoa wetu wa Njombe ni moja ya mikoa ambayo inategemewa sana katika uzalishaji. Mikoa mingine inapopata njaa sisi ndiyo watu tunaohusika katika kutoa chakula au wananchi wa Njombe ndiyo wanaosambaza chakula katika mikoa mingine tukishirikiana na Mikoa ya Ruvuma, Mbeya na Rukwa. Mikoa hii pia iweze kupewa consideration maalum katika kuhakikisha kwamba tunaipatia kipaumbele hasa kwenye upande wa pembejeo. Mara nyingi pembejeo zimekuwa zikija kwa kuchelewa, zinafika wakati tumepanda, sasa bei yenyewe iko juu, wananchi wetu hawawezi kununua kwa bei hiyo kwa sababu kipato chao ni kidogo, tunaomba bei ya mbolea ipungue, pia iwahi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Njombe huwa tunalima mara mbili, tunalima mwezi wa Sita kwenye bustani baadaye mwezi wa Kumi tunalima sehemu za milimani ambako kunazalisha magunia ya kutosha au mazao ya kutosha. Kwa hiyo, tuombe mbolea zije mapema na
ikiwezekana zianze kuja mapema mwezi wa Sita ili wananchi wetu waweze kutumia mbolea vizuri na hatimaye waweze kupata mazao vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee zao moja la chai ambalo tunalima hasa maeneo ya Lupembe na maeneo ya Luponde. Zao hili limekuwa likiuzwa kwa bei ndogo sana ukilinganisha na gharama za uzalishaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ukipiga hesabu ya mbolea inayotumika shambani, kuhudumia ule mmea mpaka unapofikia kuanza kutoa chai, kilo moja ya chai inagharimu takribani shilingi 450 na zaidi, lakini bado tunauza kwa shilingi 250, sielewi ni kwa nini zao hili limekuwa likiachwa tofauti na mazao mengine kwa hiyo tuombe wananchi wetu ili wasiendelee kuzalisha kwa hasara, angalau tupunguze baadhi ya kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali mmeshapunguza tozo la moto na uokoaji, nipongeze sana Serikali kwa jitihada hizo lakini bado bei ya kuuzia wananchi haijapanda, pamoja na kwamba baadhi ya kodi imepungua, bado bei imebaki palepale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kama kuna kodi nyingine ambazo zinafanya hili zao liuzwe kwa bei ndogo basi nazo tuziondoe ili waweze kunufaika na kilimo cha chai. Wote tunajua chai tunaitegemea sana hakuna mtu ambaye hatumii chai hapa ndani na ni zao ambalo kila mmoja
linamgusa hasa kwenye matumizi ya majani ya chai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Serikali kwenye upande wa elimu, kwa kutoa elimu bure hasa kupeleka fedha kwenye shule zetu za sekondari na msingi kwa ajili ya kugharamia elimu bure. Ni kweli kabisa baada ya kuanza kutoa fedha hizi idadi ya wanafunzi wanaoingia
darasa la kwanza imeongezeka, hata watoto wa sekondari wanaoacha yaani drop out zimepungua baada ya kuanza kupeleka hizi fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wazazi wengi walikuwa wanashindwa kulipa hizi ada na hatimaye kuwaondoa watoto shuleni na kuwarudisha
nyumbani, hasa watoto wa sekondari na shule za msingi, baada ya hii elimu bure tumeona shule nyingi zinakuwa na watoto wengi pia shule za msingi wanaoingia darasa la kwanza wameongezeka sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tatizo lipo kwenye walimu wa sayansi, pamoja na kwamba tumeajiri walimu elfu mbili na kitu, tuombe basi hao walimu wasambazwe kwenye hizi shule za sekondari ili tuwe na mkakati na ni lazima tuwe na mkakati wa kudumu wa kuhakikisha kwamba
tunawapata walimu wa sayansi wa kutosha, mkakati huu lazima tuanze mapema, tuwe na mkakati wa muda mrefu na wa muda mfupi. Tulichofanya sasa hivi ni kama muda mfupi, ni lazima tuanze kuandaa watu wetu hasa kuanzia shule za msingi kupenda masomo ya sayansi na wakienda sekondari wachukue masomo ya sayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutawezaje kufanya hivi, ni lazima sasa kule sekondari tusiweke option, tunapowaambia watoto wachague kuchukua combination za sayansi au kutosoma hasa chemistry na physics, tunafanya hawa watoto sasa waanze kukata tamaa mapema. Hivi sasa ukienda kwenye shule hizi za msingi, ukiuliza mtoto wa darasa la tano, utapenda kusoma masomo gani sekondari, atakwambia mimi nitasoma art. Nataka kuwa Mwanasiasa nataka kuwa Mwanasheria, ni lazima tutengeneze mazingira, tuwamotivate kwa kuhakikisha kwamba watoto wote wanapokwenda kidato cha kwanza… (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwa kupata fursa ya kuweza kuchangi kwenye Wizara hii ya Miundombinu. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, kwa uamuzi wake wa kununua ndege sita. Ni jambo lisilo la kawaida kwa nchi kama ya kwetu ambayo tumekuwa hatuna ndege na akaamua kununua ndege sita, kwa hiyo na mpongeza sana kwa uamuzi wake huo, ambo ni mzuri sana ambao utatusababishia Watanzania tuweze kuwa na ndege za kutosha na hatimaye kuweza kuboresha uchumi wetu wa Tanzania kwa haraka zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii, nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kwa hotoba yake nzuri ambayo inaleta matumaini katika kuboresha miundombinu. Nimpongezi Naibu wake Waziri, niwapongeze pia watendaji wa Wizara hii ya Miundombinu kwa kazi kubwa wanayoifanya hasa kuhakikisha kwamba miundombinu kwa maana ya barabara, reli na bandari na pia mawasiliano yana boreshwa kwa ajili ya kuimarisha na kuchochea uchumi wetu wa Tanzania; niwapongeze sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niwa pongeze wajumbe wa kamati ya miundombinu kwa kutuletea taarifa nzuri na kwa kazi kubwa waliyoifanya kwa kushirikiana na Wizara katika kuandaa mipango na kuishauri vizuri Wizara ili kuleta ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara hii, niwapongeze sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze kwa sababu katika taarifa yao wameeleza vizuri sana kwamba kuna baadhi ya mikoa ambayo bado haijaunganishwa na mikoa ile ya Njombe na Morogoro, mikoa ya Mbeya na Njombe, mikoa ya Katavi na Kigoma, mikoa ya Kigoma na Kagera, lindi na Ruvuma na mikoa mingine. Ukiangalia hii mikoa ambayo wameitaja ambayo haijaunganishwa ni mikoa ya uzalishaji. Ni mikoa ambayo tunaitegemea sana hasa katika kuzalisha mazao ya chakula lakini pia kuzalisha mazao ya biashara. Pia ni mikoa ambayo ina mvua nyingi sana, maana kwa kuwa ni mikoa yenye mvua nyingi lakini pia ndiyo mikoa inayozalisha chakula kwa hiyo barabara zake sio nzuri sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe katika mipango na nimeona mmeeleza na mmeiandaa vizuri sana; katika mikoa hii mmeanza kutekeleza kuhakisha kwamba inapata barabara nzuri, moja wapo ikiwa ni barabara ile ya Lupembe, barabara ambayo inasaidia sana katika kuhakikisha kwamba mazao ya biashara na mazao ya chakula kama nilivyosema yanasafirishwa. Kwa hiyo, niwashukuru kwa hilo, kwa kuhakikisha kuwa barabara yetu pia ya Lupembe inaendelea kuwekwa katika Bajeti na kuongezewa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii mwaka wa jana tuliingiza kwenye bajeti tulitengea fedha na mwaka huu pia imetengewa fedha. Sasa naomba kujua, pengine Mheshimiwa Waziri utakaposimama utatueleza vizuri, je, zile fedha ambazo zilitengwa kwenye Bunge la Bajeti mwaka jana ambapo unaishia mwaka huu, na hizi fedha ambazo zimetengwa mwaka huu je, zitajumlishwa pamoja au zile za mwaka huu ambao unaisha zimeshapitwa na wakati au hazitatumika au hazitajumuishwa na tutegemee kupata tu fedha hizi za mwaka huu?
Kwa hiyo, nitaomba utakapo kuja kufanya majumuisho basi nipewe ufafanuzi wa juu ya zile fedha ambazo tulikuwa tumetenga mwaka jana na hizi fedha shilingi bilioni mbili ambazo zimetengwa mwaka huu kama zitakuwa zitajumuishwa kwa pamoja na barabara ile ianze kufanyiwa utengenezaji au ujenzi wa kiwango cha lami. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kupongeza, kama tulivyosema nimeangalia kwenye taarifa pia mmeweza kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara nyingine, ile barabara ya kutoka Ilunda mpaka kuelekea Igongolo, ni barabara ambayo ni ya muhimu sana katika uzalishaji wa mazao, kwa maana ya uzalishaji wa wananchi wa maeneo yale. Kwa hiyo nipongeze sana kwa fedha zile ambazo zimetolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe badala ya kuendelea kutenga fedha kwa kiwango cha kokoto ni vizuri tuanze kujielekeza kutenga fedha kidogo kidogo kuanza kutengeneza kidogo kidogo lami na hatimaye barabara nzima zitakuwa zimekamilika au tuanze kutengeneza zile sehemu ambazo tunafikiri kwamba ni korofi, sehemu ambazo wakati wa kifuku wananchi/wakulima wetu wadogo wadogo hawawezi kupitisha mazao yao yakafikia kwenye masoko basi angalau zianze kujengwa maeneo hayo kwa kiwango cha lami na hatimaye tutaweza kumaliza barabara nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukisubiri tu fedha itakuwa ni ngumu lakini tukianza na hizo fedha ndogo ambazo tunatengenezea vifusi vya kokoto, tukaanza kutengeneza kiwango cha lami kwenye maeneo yale ambayo ni korofi na hatimaye barabara zote zitatengenezwa kirahisi zaidi na zitaweza kupitika wakati wote hata wakati ule wa mvua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie pia kwenye upande wa mawasiliano. Imeelezwa hapa kwamba maeneo mengi ya vijijini bado mawasiliano ni shida, bado hayafikiki mawasiliano na maeneo haya ya vijijini ndiyo maeneo ambayo tunayategemea, kama tulivyosema, kwenye uzalishaji wa mazao ya biashara na chakula; kwa kuwa maeneo haya hayana mitandao ya simu au hayajajengwa minara ya simu. Kwa mfano katika Jimbo langu la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, kuna kata tano hazina mawasiliano. Kuna kata za Ikondo, Ninga, Mfiliga, Idamba na Ukalawa hazina mawasiliano, kwa hiyo vijiji vyote vya maeneo hayo simu hazipatikani kwa urahisi zaidi. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri maeneo hayo tuweze kujengewa minara ili wananchi wale waweze kupata mawasiliano kirahisi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nichangie juu ya suala mtambuka. Niwapongeze Wizara kwa uamuzi wa kuanzisha mafunzo maalum kwa wakandarasi wa kike, mafunzo hasa yanayohusika na ukarabati na matengenezo
ya barabara na uandaaji wa zabuni. Hii itasaidia akina Mama wengi kujiunga na ukandarasi au kusoma masomo ya ukandarasi, masomo ya sayansi, lakini pia itawasaidia wanafunzi wetu wa shule za sekondari kuanza kupenda masomo ya sayansi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ilivyo sasa hivi wanafikiri kwamba ukandarasi au uhandisi au u-engineer ni kwa ajili ya wanaume tu. Kwa hiyo tukiwawesha hawa na wanapoenda huko kwenye maeneo haya ya ujenzi wa barabara wakiwaona basi watahamasika kusoma masomo ya sayansi na kuhakikisha kwamba wanafaulu vizuri, na tutakuwa na wanawake wengi ambao wanakuwa ni Ma- engineer na hatimaye kuwa na ma-engineer wa kutosha kuliko ilivyo sasa hivi, ma-engineer wengi ni wa kiume kuliko ma-engineer wa kike. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine nichangie juu ya ajira hasa ajira za vibarua, wale ambao they are not trained kwenye maeneo huko ambako shughuli za ujenzi wa barabara zinaendelea. Niombe tuweke utaratibu wa kuwaangalia wale watu wanaowekwa kwenye maeneo ambako miradi hii inatengenezwa. Tukifanya hivi itasaidia kuwapa ajira vijana wa maeneo husika ambako barabara zinajengwa, lakini pia itawafanya hawa vijana wasiharibu miundombinu ya barabara hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine vijana au watu wa maeneo yale wanaharibu kwa sababu wanaona kama ile barabara kwao hawajanufaika, wanapoona wajenzi wa barabara au wanaoshiriki kutoa labour force ya zile ambazo hazihitaji wasomi wanatumika watu wa kutoka maeneo ya mbali. Na kuna maeneo mengine wamekuwa wakiiba vifaa vya ujenzi au waki- vandalize vifaa vya ujenzi kwa sababu tu wao hawajashirikishwa katika ujenzi wa barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tukiwatumia vijana wa maeneo husika, maeneo ambako mradi unafanyika itawasaidia vijana wenyewe kuanza kupenda shughuli zile na kuhakikisha kwamba wanakuwa walinzi wa vifaa na mali zilizoko katika maeneo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, ahsante sana.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kuunga mkono hoja iliyoletwa na Serikali. Nampongeza Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii kwa utumishi uliotukuka katika kuwasaidia Watanzania, katika kuwa na afya na kutatua changamoto mbalimbali za kijamii zilizopo chini ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu magari ya wagonjwa (ambulance); magari haya ni muhimu sana kama ilivyo muhimu kuwa na dawa za kutosha, vifaa tiba vya kutosha. Pia ni muhimu kila hospitali na baadhi ya vituo vya afya vilivyopo maeneo ya vijijini ndiyo vinavyohudumia watu wengi sana ambao wanategemea kupata matibabu katika vituo hivi pekee tofauti na maeneo ya mjini ambako kuna hospitali na vituo vya afya visivyo vya Serikali. Mfano, katika Jimbo la Lupembe Halmashauri ya Wilaya ya Njombe eneo hili lina takribani watu zaidi ya 100,000 lakini ina vituo vitatu tu vya afya na hakuna hospitali yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wagonjwa wamekuwa wakitembea umbali mrefu kwa ajili ya kupata matibabu kwenye kituo cha afya kilichopo Lupembe umbali wa kilometa 75 toka Hospitali ya Kibena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kituo kipya cha Kichiwa kipo umbali wa kilometa 50 toka Hospitali ya Kibena na kituo cha Sovi ambacho kipo umbali wa kilometa 45 toka Hospitali ya Kibena. Katika Halmashauri yetu tumekuwa tukipoteza akina mama wengi kwa kucheleweshwa kupata upasuaji kutokana na kutokupata msaada wa usafiri kwa ajili ya kupelekwa Hospitali ya Kibena kwa ajili ya upasuaji. Hivyo tunaomba tupewe gari angalau moja kwenye vituo hivi vitatu kwa ajili ya kuwasaidia usafiri akina mama wajawazito na wagonjwa mahtuti ili kuwahi matibabu au huduma kwenye Hospitali ya Kibena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Hospitali ya Wilaya, Jimbo letu na Halmashauri ya Wilaya ya Njombe haina hospitali. Tumeanza jitihada za kujenga hospitali ya Wilaya. Wananchi kwa kutambua umuhimu wa kuwa na hospitali ya Wilaya, wamejitolea eneo lao lenye ukubwa wa ekari 52 ili eneo hili litumike kwa ajili ya ujenzi wa hospitali. Tunaomba Serikali itusaidie kupata fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wazee ambao ni wazazi wetu ambao sisi watoto wao tuna wajibu wa kuwasaidia kwa malazi, mavazi, chakula na kuwahudumia pale wanapokuwa na matatizo ya kiafya. Wazee wengi wanafariki kabla ya muda wao kutokana na ugumu wa maisha na msongamano wa mawazo unaotokana na watoto wengi hawatunzi wazazi wao, hata kama watakuwa na uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zilizoendelea wazee wanatunzwa vizuri na Serikali kwa kushirikiana na watoto wao. Hii inawafanya waishi miaka mingi tofauti na Tanzania na nchi nyigine za Afrika. Hivyo basi, napendekeza Serikali ije na sheria itakayotutaka Watanzania kuhakikisha kwamba wanawatunza wazazi wao hasa wanapokuwa wazee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia mara nyingi watoto wakipata kipato huwa wanawasahau wazazi waliowalea, wazazi wanataabika vijijini bila chakula na makazi duni wakati wao wakiwa na maisha mazuri. Hivyo sheria ikitungwa itawabana watoto wao kuwa na wajibu wa kuwalea wazazi wao, angalau kwa kuwapa huduma za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi hasa maeneo ya vijijini.Mara nyingi watumishi wa afya wakianzia kazi mjini huwa hawapo tayari kuhamia vijijini pale wanapopata uhamisho wa kwenda vijijini. Hivyo Serikali iangalie uwezekano wa kuwafanya watumishi wawe flexible kwenda popote atakapopangiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali ipeleke watumishi wa afya katika maeneo ya vijijini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Njombe. Pia pale penye upungufu wa watumishi au watumishi kutakiwa kufanyakazi masaa ya ziada tunaomba Halmashauri na Wizara kuwalipa malipo yao ya kazi za ziada au on call allowances wapewe na ikiwezekana Serikali iwaongezee, shilingi 25,000 ni ndogo sana. Serikali ione uwezekano wa kuongeza kiwango hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mimba za utotoni na ukatili wa watoto; pamoja na tatizo hili kuchangiwa na mila na desturi pamoja na imani za kishirikina, pia wazazi kutotimiza wajibu wao wa malezi inachangia watoto wengi kupata mimba wakiwa na umri mdogo. Kila mzazi anatakiwa na ana wajibu wa kumlea mtoto wake katika maadili mema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazazi wengi wanaacha watoto wao walelewe na house girls na television, vitu hivi ndivyo vinavyochangia watoto wengi kukosa malezi bora. House girls na television ndio wamekuwa walimu wa watoto hususani kwenye upande wa ngono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine linalosababisha mimba za utotoni na ukatili kwa watoto ni umbali wanaotembea watoto wetu kwenda shuleni. Mtoto anayetembea zaidi ya kilometa tano kwenda shule ya msingi au sekondari, ana hatari kubwa ya kukumbana na vishawishi vya ngono kuliko mtoto anayetembea chini ya kilometa tano. Shule nyingi zilizopo maeneo ya vijijini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Njombe wapo hatarini kujiingiza kwenye vitendo hivyo na hatimaye kupatikana na ukatili wa kijinsia au mimba za utotoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kutatua matatizo ya mimba za utotoni ambazo kwa sasa zinasababishwa na vijana wanaotoa msaada wa usafiri (lift) bodaboda na magari na kuwafanyia ukatili watoto wetu, ni vizuri Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Wizara ya TAMISEMI, tuje na mpango wa kujenga hostels kwenye shule zetu za msingi na sekondari ili kuwaepusha watoto wetu kuingia kwenye vishawishi vitakavyopelekea kwenye matatizo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu huduma za damu salama, bado kuna changamoto ya watu kujitolea kuchangia damu na maeneo mengine hasa vijijini wananchi wengi hawapo tayari kuchangia damu mpaka walipwe. Hivyo Serikali iendelee kutoa elimu kwa wananchi waishio vijijini juu ya umuhimu wa kuchangia damu. Hii itaongeza mwamko wa wananchi waishio vijijini kuchangia damu bila malipo pale wanapoombwa kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Waziri wa Maji na Naibu Waziri pamoja na Watendaji wote wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha Watanzania wanapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai; bila maji hakuna maisha ya binadamu wala viumbe hai vingine. Tatizo la uhaba wa maji nchini na duniani linazidi kuongezeka. Hii kama wataalam wanavyosema, inaashiria, vita kubwa duniani itakayotokea itakuwa ni vita ya kuvigombea (scramble for) maji. Hivyo ni muhimu kwa nchi yetu, Serikali yetu kupanga vizuri juu ya mipango mizuri ya usambazaji maji kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe bado tuna vijiji vingi havina maji safi na salama. Mfano vijiji vya Matiganyora, Nyombo, Lole, Igongolo, Tage, Mende, Kichiwi, Ilengititu, Ibiki, Kidegembye, Havanga, Iyembele, Isoliwaya, Kanikelele, Iwafi, Lima, Welele, Ikang’asi na Igombola havina maji. Tunaomba vijiji hivi navyo viwekwe kwenye mpango wa kupewa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi mingi ya maji imekuwa ikitekelezwa kwa kuchelewa sana na wakati mwingine imekuwa haikamiliki vizuri. Hii ni kutokana na kucheleweshwa na taratibu za manunuzi na zabuni. Mara nyingi wanaochelewesha zabuni hizi na taratibu za manunuzi ni watendaji wetu waliopo kwenye Halmashauri zetu. Hivyo nadhani umefika wakati Serikali iwapime Watendaji wetu waliopo kwenye Halmashauri kwa idadi ya miradi ya maji iliyokamilika ndani ya muda ndani ya Halmashauri zao. Mfano, Mhandisi wa Maji wa Halmashauri atabaki kwenye nafasi yake kwa kupimwa kwa speed yake ya kusimamia miradi ya maji, ubora wa kazi ilivyofanyika, utoaji wa elimu bora kwa watumiaji wa maji kupitia Kamati za Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado fedha inayotengwa kwenye Mfuko wa Taifa wa Maendeleo ya Maji haitoshelezi mahitaji ya maji safi na salama nchini. Hivyo, nami naungana na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba iongezwe sh.50/= kutoka kwenye kila lita ya mafuta. Tatizo la maji mijini na vijijini linawaingizia gharama kubwa wananchi, kutokana na gharama ya kununua maji kwa wale wanaouza maji; gharama ya muda ambao akinamama wanatumia kwenda kutafuta maji; gharama kubwa wananchi wanazotumia kutibu magonjwa yanayotokana na ukosefu wa maji safi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukabiliana na tatizo la ukosefu wa maji nchini ni muhimu tuongeze sh.50/= kwenye bei ya mafuta ili fedha hizi ziende kwenye mfuko huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu tumejaliwa kuwa na vipindi vya mvua ya kutosha kila mwaka. Maji yanayotokana na mvua hayatumiki vizuri, yamekuwa yakipotea tu. Ni muhimu Serikali ipitishe sheria ndogo ya uvunaji wa maji toka kwenye majengo yetu, pia maeneo ambayo yana mvua nyingi. Ni vizuri tukaanzisha utaratibu wa kujenga mabwawa ya maji ili yatumike wakati wa kiangazi kwa shughuli mbalimbali, pia uvunaji wa maji maeneo ya mvua nyingi itasaidia kupunguza mafuriko maeneo ambayo maji haya huelekea, yaani maeneo ya uwanda wa chini (low land).

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi nami kuchangia kwenye Wizara hii, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayofanya kuhahakisha kwamba wananchi wanapata makazi bora lakini pia kutatua migogoro ya ardhi nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niseme mambo machache hasa kuhusu watumishi wa Idara ya Ardhi. Halmashauri nyingi hasa hizi Halmashauri za Wilaya, Halmashauri za vijijini hizi hazina watumishi wa kutosha wa idara hii ya ardhi, hasa Maafisa Ardhi wateule. Wilaya ya Njombe mpaka sasa hatuna Afisa Ardhi Mteule, tukitaka kusaini hati tunamtumia Afisa Ardhi Mteule wa Halmashauri ya Mji, kwa hiyo, mara nyingi tunapotaka kusaini hizi hati zimekuwa zikichelewa kwa sababu na yeye ana majukumu ya Halmashauri yake. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri ukishirikiana na TAMISEMI tuweze kupata Afisa Ardhi aweze kutusaidia kuweza kupata hati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hati za viwanja zimekuwa zikichelewa na kwenye Halmashauri yangu tuna wananchi wengi ambao wana mashamba ya chai na wangependa wapate hati ambazo zingeweza kutumika kwa ajili ya kupata dhamana kwenye mikopo na sehemu mbalimbali, lakini zimekuwa zikichelewa kwa sababu tu hatuna Afisa Ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzoefu unaonyesha kwamba maeneo yote ambayo yana Maafisa Ardhi Wateule ndio maeneo ambayo migogoro inapungua sana, kwa hiyo, wanafanya kazi kubwa sana za kupunguza migogoro, lakini maeneo ambayo yanakuwa hayana Maafisa Ardhi Wateule migogoro inakuwa mingi. Kwa hiyo, tukiajiri Maafisa Ardhi Wateule wa kutosha katika Halmashauri zetu naamini migogoro mingi itapungua. Mfano ni pale Halmashauri ya Mji wa Njombe, tulikuwa na migogoro sana ya ardhi miaka ya nyuma, lakini sasa hivi imepungua na inaendelea kupungua kwa sababu tuna Afisa Ardhi ambaye anafanya kazi vizuri sana. Tunaomba Halmashauri zetu zote ziwe na Maafisa Ardhi Wateule na maafisa wengine wawepo ili kasi ya upimaji wa ardhi na kasi ya utoaji wa hati iweze kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu mikopo ya nyumba. Nampongeza Waziri kwamba kuna mpango wa kuanza kukopesha nyumba kwa wenye vipato vidogovidogo, mpango huu umejikita sana kwenye maeneo ya mijini, tuende vijijini ambako kuna wakulima wadogo wadogo na vijana ambao wanafanya kazi za bodaboda na shughuli ndogondogo waweze nao kumiliki nyumba. Tufuate utaratibu ule wa VIGUTA ambao wanajenga nyumba za bei rahisi sana. Wanajenga nyumba mpaka za shilingi milioni 15, shilingi milioni 25 lakini wanajenga nyumba za ghorofa moja mpaka za milioni 60 na wamejenga maeneo ya Kibaha pia sasa hivi wanajenga maeneo ya Dodoma.

Kwa hiyo, twende vijijini hawa wakulima wetu wadogo wanahitaji nyumba, naamini kwamba kupitia shughuli zao za kilimo, kupitia shughuli zao za bodaboda na ujasiriamali mdogomdogo wakiwekewa utaratibu mzuri wanaweza wakamiliki hizi nyumba, wanaweza wakajenga nyumba na wakarudisha hizo fedha kupitia hizo shughuli zao za kila siku kwa maana ya bodaboda au ujasiriamali na kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia juu ya bei viwanja. Bei ya viwanja bado iko juu kwenye baadhi ya maeneo. Kuna maeneo hasa viwanja vile ambavyo vinapimwa na makampuni au mashirika mbalimbali kwa kushirikiana na Halmashauri, viwanja hivi vinauzwa bei ya aghali sana. Kwa mfano, utakuta kiwanja kinauzwa shilingi milioni 10, shilingi milioni 20 eti kwa sababu tu barabara imetengenezwa au maji yamepelekwa. Ukiangalia utakuta kwamba wananchi wa kipato cha chini ambao wana uwezo mdogo wa kupata hizi fedha hawawezi kumiliki hivi viwanja kwa sababu ni vya bei ya juu sana. Tuweke utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba tunathibiti bei za hivi viwanja, tukiacha hivi makampuni haya kama hali iliyopo utakuta kwamba wananchi wa chini watashindwa kumiliki viwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia wanaoweza kununua hivi viwanja shilingi milioni 10, shilingi milioni 20 ni wale watu wenye uwezo tu, ni wale watu wenye kipato cha juu. Utakuta hawa wananchi wenye kipato cha chini wanazidi kwenda pembezoni, wanaondoka katika maeneo yale kwa sababu hawana uwezo wa kumiliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali kwa jinsi inavyotekeleza majukumu yake. Nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mawaziri wote na Watendaji wote wa Serikali kwa kuwa na sense of duty.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha chai; zao la chai ni zao ambalo lilikuwa linaingiza fedha nyingi za kigeni miaka ya 1970 na kabla ya miaka 1990. Mfano, chai ya Lupembe ipate soko kubwa na ikawa namba moja kwa ubora duniani. Katika miaka ya hivi karibuni baada ya kukaribisha wawekezaji uzalishaji ukapungua na kupelekea kupoteza soko lake. Hii ni kutokana na kutokuwa na usimamizi mzuri wa zao hili. Tunaomba Serikali ione umuhimu wa kusaidia kufufua zao hili kwani kwa Mikoa ya Njombe, Mbeya na Tanga zao hili huajiri watu wengi sana mashambani na viwandani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu kwa Serikali kufuatilia uzalishaji wa zao hili toka shambani mpaka sokoni, mchakato mzima toka uhudumiaji wa shamba, uchumaji, namna biashara inavyofanyika toka kwa mkulima na wenye viwanda na uzalishaji wa majani mabichi, kwa majani makavu na hatimaye soko lake la nje. Ilivyo sasa wakulima wadogowadogo wanadhulumika sana kupitia mizani wanayopimia mashambani. Chai ikizalishwa zaidi ya mahitaji ya viwanda, wakulima wanaambiwa chai ni chafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bei ya chai. Bado bei elekezi ni ndogo sana, hivi karibuni bei iliyotangazwa ni ongezeko la Sh.35 hivyo kupanda toka Sh.230 mpaka Sh.250 na Sh.265 mpaka Sh.285 kwa majani mabichi. Bei hii haimnufaishi mkulima, gharama za uzalishaji ni kubwa kuliko gharama za kuzuia majani mabichi. Kwa sasa hivi, gharama za kuzalisha kilo moja ya majani mabichi takriban au wastani wa Sh.400 mpaka Sh.450 lakini bei ya kuuzia majani mabichi ni Sh.230 mpaka Sh.250. Bei hii ni bei nyonyaji kwa wakulima. Naomba Serikali hasa Wizara ya Kilimo kusimamia na kufuatilia bei ya zao hili la chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu ya kuelekea kwenye maeneo ya uzalishaji chai. Barabara zinazoelekea kwenye mashamba ya chai ni mbovu sana, barabara hazipitiki wakati wa mvua. Hii pia inachangia kupoteza ubora wa chai. Zao hili la chai huzalishwa kwa wingi wakati wa mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huu ili kupata ubora wa zao hili barabara zilitakiwa ziwe nzuri lakini mara nyingi zimekuwa hazitengenezwi. Serikali iangalie uwezekano wa kuwa na mfuko rasmi wa barabara za maeneo ambako chai inazalishwa kama ilivyokuwa zamani, wakati wa Mamlaka ya Chai, barabara za mashamba ya chai zilitengenezwa na fedha kutoka World Bank na ndipo chai ilipopata ubora mzuri katika soko la dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mbolea. Bado kuna tatizo kubwa katika usambazaji wa mbolea. Mfano, katika Mkoa wa Njombe bei ya mbolea pamoja na kutangaza bei elekezi bado kumekuwa na ujanja ujanja wa mawakala wadogo wa mbolea. Kilichotokea mbolea hizi zilifika kwa wakati katika Miji ya Njombe na Makambako na zimekuwa zikiuzwa kwa bei elekezi yaani Sh.44,000 (CAN), mpaka elfu Sh.52,900 (UREA).

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, mbolea hizi hazijawahi kupelekwa vijijini na kuuzwa kwa bei hizo, wafanyabiashara wanasema hawawezi kupeleka maeneo ya Lupembe, Kichiwa na maeneo ya vijiji vilivyo nje ya barabara ya lami. Mbolea hizi zimekuwa zikiuzwa kwenye maeneo ya vijijini kwa bei zaidi ya ile bei elekezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi UREA ni Sh.61,000, wakulima wanatakiwa kununua mjini na kuisafirisha mpaka mashambani (vijijini) hivyo gharama kuongezeka mara dufu. Tunaiomba Serikali ipeleke mbolea hizi kwenye Makao Makuu ya Kata au Tarafa ili kuwarahisishia wakulima gharama kubwa za usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maji. Tatizo la maji vijijini bado ni kubwa, mfano; katika Jimbo la Lupembe kuna zaidi ya vijiji 25 havina maji. Pamoja na Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe kuongoza Kitaifa kwenye usafi wa mazingira na vyoo bora lakini vijiji vyake havina maji safi. Njombe ni eneo ambalo limezungukwa na mito mingi na mito hii inamwaga maji yake katika Mto Rufiji, hivyo Njombe ni catchment area ya Mto Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia eneo hili kutokana na kutokuwa na maji milimani ambako ndiko yaliko makazi yao hulima mabondeni, hivyo ili kulinda vyanzo vya maji katika Mkoa huu ni muhimu kuwapelekea maji wananchi hawa ili waanzishe bustani za mbogamboga milimani (kilimo cha umwagiliaji) tusipofanya hivyo mipango ya kuwa na miradi mikubwa hasa ule wa Rufiji utaathiriwa na kilimo cha mabondeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ione umuhimu wa kuwapelekea maji safi ili iwe rahisi kuwashawishi wananchi kulima bustani zao milimani ambapo watatumia maji bomba kumwagilia bustani zao.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli; Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu; Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa na Baraza lote la Mawarizi kwa namna wanavyofanya kazi usiku na mchana kwa ajili ya maendeleo ya Tanzania na Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo endelevu ni maendeleo ya watu na siyo vitu. Maendeleo ya watu huonekana katika viashiria kama vile pato la mtu mmoja mmoja, fursa ya kupata huduma muhimu kama elimu, afya, mavazi, maji safi, umeme na huduma za usafiri. Naipongeza sana Serikali kwa kuhakikisha kwamba maendeleo ya watu yanapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo yote makubwa yanayofanyika nchini yamelenga kuboresha maisha ya Watanzania. Mfano, elimu bure, maboresho mbalimbali katika Sekta ya Afya, miundombinu ya barabara, reli, viwanja vya ndege na mengine mengi yanaendelea kufanyika na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi maridadi wa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya ahadi za viongozi wa Kitaifa hususan Rais, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu, mpaka sasa hazijatekelezwa. Kwa namna moja au nyingine zinakatisha tamaa wananchi kwa kuona baadhi ya ahadi hazitekelezwi kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu hususan barabara, katika Jimbo la Lupembe Halmashauri ya Njombe DC kuna barabara ya Lupembe, yaani Kibene – Lupembe – Madeke (kilometa 126) iliahidiwa na Mheshimiwa Jakaya Kikwete mwaka 2010 na kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2015 iliahidiwa kuwa barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Mwaka 2016/2017 na mwaka 2017/2018 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania liliipangia bajeti barabara hii kwa ajili ya kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami kilometa 50, lakini mpaka leo hii tukiwa tunamaliza mwaka wa fedha, barabara hii haijaanza kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni muhimu sana kwani ndiyo barabara pekee inayounganisha Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Morogoro kupitia Mlimba. Pia kiuchumi barabara hii ndiyo inayoongoza kwa kuwa na magari mengi yanayosafirisha mazao mbalimbali katika Mkoa wa Njombe. Mazao yanayosafirishwa na barabara hii ni mbao, chai, mahindi, maharage, matunda mbalimbali na viazi. Hivyo tunaomba barabara hii itengenezwe kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishukuru Serikali kwa kuhakikisha kwamba dawa zinapatikana katika hospitali zote. Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ni miongoni mwa Halmashauri ambazo hazina Hospitali za Wilaya. Halmashauri hii ina Vituo vya Afya vinne; Kituo cha Lupambwe, Kichiwa, Matembwe na Sovi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa ukarabati wa Vituo vya Afya, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ilikuwa ni miongoni mwa Halmashauri ambazo ziliahidiwa kupewa shilingi milioni 500. Nami kama Mbunge wa Jimbo, nilipewa taarifa na kuoneshwa orodha ya Halmashauri zilizopata shilingi milioni 500. Cha kushangaza, fedha zilipotoka hazikuletwa kwenye Halmashauri yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kufuatilia sana, nikaambiwa tutaingiziwa kwenye mpango wa shilingi milioni
400. Fedha zilipotoka, bado Halmashauri yangu haijapata fedha hizo wakati kuna Halmashauri zimepata fedha za ukarabati kwa Vituo vya Afya viwili, nyingine vitatu. Juzi juzi tumeona baadhi ya Halmashauri zimepata vituo mpaka vitano. Halmashauri hii licha ya kuwa ina changamoto ya usafiri, vituo vyote havina hata gari la wagonjwa, lakini pia kwenye mgao wa magari tumekosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kwamba resources tulizonazo hazitoshi kusambaza kwenye Halmashauri zote, lakini angalau basi wale wenye matatizo makubwa zaidi angalau wawe wanafikiriwa. Fedha ni kidogo lakini kilichopo angalau tugawane wote. Wananchi wa Jimbo langu wanavyopata taarifa zinazoonesha Halmashauri nyingine zimepata fedha za ukarabati na miradi mingine ambayo viongozi wetu wameahidi na wao hawapelekewi hizi fedha, wanajisikia vibaya na kuona kama wanatengwa. Hivyo naiomba Serikali angalau itusaidie fedha hizi za ukarabati wa Vituo vya Afya vya Lupembe, Kichiwa na Sovi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu. Napongeza jitihada za Serikali katika kuhakikisha kwamba vijijini na mijini kunakuwa na umeme. Hii itasaidia sana maendeleo ya viwanda nchini. Katika Jimbo langu kuna maeneo tayari wananchi wameitikia kaulimbiu ya Tanzania ya viwanda kwa kununua viwanda. Mfano Kijiji cha Ninga wamenunua Kiwanda cha Sembe chenye uwezo wa kuchakata tani 12 mpaka 20 kwa siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ni kwamba kijiji hiki hakina umeme pamoja na ahadi za muda mrefu kwamba wataletewa umeme. Pia tuna Kijiji cha Madeke walinunua Kiwanda cha Kusindika Matunda lakini hakuna umeme. Pamoja na jitihada za Serikali kupitia mpango wa REA, lakini kasi yake bado ni ndogo. Hivyo tunaomba maeneo haya yapelekewe umeme haraka ili viwanda hivi vianze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naipongeza Serikali hasa Waziri Mkuu kwa kufika Lupembe na kutatua baadhi ya changamoto mwaka 2017. Naomba Mwenyezi Mungu amjalie afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja iliyopo mezani.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii. Nianze kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Wazri kazi kubwa ambazo wanazifanya kwa ajili ya kuboresha afya za Watanzania nawapongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda hautoshi nichangie kidogo juu ya afya na usafi wa mazingira. Naipongeza Serikali kwa kuanzisha hii kampeni ya usafi wa mazingira na kuhakikisha kwamba Watanzania wanatumia vyoo bora. Ni dhahiri kwamba kama inavyooneshwa kwenye taarifa matumizi ya vyoo bora imeongezeka toka 1,996,413 mwezi Juni, 2017 na mpaka hadi sasa hivi kuna vyoo milioni 2,414, 094 ilipofika Desemba. Nipongeze sana ni dhahiri kwamba tunapoboresha vyoo ni kwamba tunapunguza magonjwa ambayo yanasababishwa na uchafu. Kwa hiyo, ninapongeza kwa kufanya hivyo maana yake tunapunguza gharama za kutibu haya magonjwa ambayo yanatokana na kukosa vyoo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmshauri ya Wilaya ya Njombe imekuwa ikiongoza katika usafi huu wa vyoo na mazingira bora toka mwaka 2013, ilikuwa ya kwanza mwaka 2014 kijiji cha Wagenyi kilikuwa cha kwanza na Halmashauri ilikuwa ya kwanza, mwaka 2015 kijiji cha Image kilikuwa kijiji cha pili na Halmashauri ilikuwa ya pili, mwaka 2016 kijiji cha Wanginyi kilikuwa cha kwanza, Matiganjola kikawa cha pili Sovi cha tatu na Halmashauri yangu ilikuwa ya kwanza ninaishukuru Serikali ilitupatia zawadi ya gari Land Cruiser.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2017 kijiji changu ambako mimi natoka ninakoishi kijiji cha Kanikere kiliongoza nchi hii na kuwa cha kwanza, lakini kijiji cha pili kilikuwa kijiji cha Nambara cha kutoka Mara, kijiji cha tatu kilikuwa kijiji cha Lyalalo kutoka Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe na kijiji cha nne kilikuwa cha Image.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka nijue vizuri Waziri utakaposimama utueleze vizuri maana yake nilikuwa napiga hesabu hapa, hesabu ndogo tu ilitumika hapa ukipiga hesabu utakuta kwamba Halmashauri ambaye ilitakiwa iwe ya kwanza ni Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, maana kuna vijiji vitatu vipo namba moja, namba tatu na namba nne lakini cha kushangaza tukaambiwa kwamba sisi ni namba mbili Halmashauri ambayo ina kijiji kimekuwa namba moja. Sasa nataka nipate ufafanuzi ni kwa nini Halmashauri tena haikuwa ya kwanza wakati kuna vijiji namba moja, kijiji namba tatu, kijiji namba nne kinatoka Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, lakini kijiji cha Nambara ambacho kipo Meru kilikuwa cha pili na Halmashauri ikawa ya pili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika simple arithmetics naona kama kidogo inagoma, basi utanisaidia mwishoni kutoa ufafanuzi ilikuwaje na hesabu zilipigwaje Halmashauri yangu ikawa ya pili badala ya kuwa wa kwanza. (Makofi)

Pia ninaipongeza Serikali kwa kuja na mpango huu wa hasa huduma ya CHF kuhakikisha kwamba tunatoka kwenye CHF ambapo mwananchi alikuwa anakatia kwenye kituo cha afya au zahanati hapo na anatakiwa kutiwa kwenye eneo lake husika tu na kuna maeneo mengine tunaenda mbali tukawa tunatibiwa kwenye Kata kwenye Halmashauri moja ndani ya Halmashauri anaweza akatibiwa sehemu yoyote ile, lakini sasa hivi Serikali imeenda mbali zaidi kuhakikisha kwamba kwa mpango huu unoitwa ICHF sasa wananchi wataweza kutumia hiyo CHF iliyoboresha kutibiwa ndani ya Mkoa kwa maana wataweza kutibiwa mpaka kwenye Hospitali ya Rufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni hatua kubwa sana naipongeza sana Serikali, naamini kwamba kupitia mpango huu wananchi wetu hasa ambao wanaishi maeneo ya viijini ambao kwao tiba imekuwa ni changamoto kubwa, hasa wanapotoka nje ya Halmashauri sasa watapata matibabu kirahisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishukuru Serikali na niunge mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nianze kwa kuwapongeza sana Mawaziri wanaosimamia Wizara, hii kwa maana ya Waziri Mheshimiwa Profesa Mbarawa, Mheshimiwa Nditiye na Mheshimiwa Kwandikwa na Makatibu Wakuu wote na watumishi wote wa Wizara hii ya Ujenzi kwa namna wanavyofanya kazi usiku na mchana kuhakikisha kwamba miundombinu mingi inatengenezwa hasa barabara na mambo mengine ya viwanja vya ndege na bandari. Niwapongeze sana, wanafanya kazi kubwa sana ambayo itasaidia kusukuma maendeleo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haipingiki ni kwamba tunavyoboresha barabara, tunavyoboresha viwanja vya ndege, tunavyoboresha bandari na miundombinu mingine tunachochea kwa kasi kubwa sana maendeleo. Kwa hiyo naipongeza sana Serikali, inafanya kazi kubwa sana. Tayari tumeshaona maeneo ambako barabara za lami zimefunguliwa, maeneo ambako kuna ujenzi wa reli na maeneo mengine ambapo miundombinu inatengenezwa, tayari kasi ya maendeleo imeanza kuonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali tuendelee bila kukata tamaa na kusikiliza maneno ya watu ambao wanabeza maendeleo haya. Tumwombe Mheshimiwa Rais aendelee kutusaidia kuhakikisha kwamba Watanzania tunatoka hapa tulipo tunaenda mbali zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuongelea kuhusu Jimbo langu hasa barabara ile ya Kibena – Lupembe – Madeke - Morogoro. Barabara hii inaunganisha Mkoa wa Njombe na Morogoro na ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu, lakini pia kwa uchumi wa Mkoa wa Njombe. Katika eneo ambako barabara hii inapita, eneo lote la Lupembe na Jimbo zima tunazalisha mbao kwa wingi sana. Mbao mnazoziona Dodoma asilimia 40 zinatoka kule Lupembe lakini eneo hili pia tunazalisha nguzo za umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema hapa kwamba tunataka kila kijiji kiwe na umeme, nguzo zinatoka katika maeneo haya kwa asilimia kubwa sana. Eneo hili pia tunazalisha chai kwa wingi sana, kahawa, mahindi, maharage na aina zote za matunda kama vile parachichi, papai, nanasi, ndizi na matunda mengine mengi. Eneo hili lina mvua nyingi, takribani miezi nane katika kipindi cha mwaka mzima ni kipindi cha mvua. Kwa hiyo, unaweza ukaona kwa namna gani ni muhimu sana hizi barabara za maeneo haya ziweze kutengenezwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka 2016/2017, barabara hii ilipangiwa shilingi bilioni nane kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami na mwaka wa 2017/2018, tulipanga shilingi bilioni mbili na mwaka huu nashukuru sana Wizara na Serikali kwa ujumla tumepangiwa shilingi bilioni tano. Niombe sana bado barabara hii haijatangazwa kwa maana ya zabuni, haijatangazwa ili kuweza kumpata mkandarasi ili aanze kutengeneza barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba upembuzi yakinifu umeshakamilika, usanifu umeshafanyika lakini bado ujenzi wake haujatangazwa. Niombe sana Wizara hii ya Ujenzi itusaidie ili barabara hii iweze kutengenezwa kwa kiwango cha lami na hatimaye tuweze kusafirisha mazao haya niliyoyataja kwa urahisi zaidi ili yaweze kufikia soko kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukipoteza fedha nyingi sana hasa kwenye mazao haya ya chai, mbao na mazao ya matunda kama nilivyoyataja. Kwa mfano, mwaka huu tu kuanzia Januari mpaka sasa hivi mwezi wa kwanza wananchi wa Madeke walipakia nanasi tani 40 kwenda kuuza sokoni lakini tani hizi zote 40 zimeozea njiani kwa sababu ya ubovu wa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo katika barabara hii yameharibika, magari hayawezi kupita mfano maeneo ya Mtakuja, baadhi ya maeneo ya Kidegembye na maeneo mengine mengi tu. Kwa hiyo, unaweza ukaona jinsi tunavyopoteza uchumi katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki mbili zilizopita tumepakia maparachichi tani 30 katika vijiji viwili tu, unaweza ukaona ni shilingi ngapi hizo. Baada ya kuwaka jua kidogo tu siku mbili, tatu tukaweza kusafirisha tani 30 za parachichi kutoka kwenye vijiji viwili tu na parachichi kilo moja ni Sh.1,150. Kwa hiyo, unaweza ukaona ni namna gani hii barabara inavyochelewa kutengenezwa tunavyopoteza fedha nyingi na wananchi wanavyoingia hasara kutokana na ubovu wa barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali barabara hii tuipe kipaumbele ili angalau mwaka huu mara baada ya kupitisha bajeti hii, basi itangazwe, tupate mkandarasi aanze kutengeneza barabara hii. Kwa sababu tukiunganisha Mkoa wa Njombe na Morogoro na Mkoa wa Morogoro ni wazalishaji wakubwa sana naamini pato la Taifa litaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukiunganisha kwa mfano, Mkoa wa Njombe na Morogoro, tukaunganisha Mkoa wa Njombe, Makete na Mbeya, tukaunganisha Mkoa wa Njombe kupitia Ludewa na mikoa mingine kimsingi tutapata maendeleo makubwa sana kwa sababu haya ndiyo maeneo yanayotegemewa kwa chakula na ndiyo maeneo yenye uchumi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri hii barabara wananchi wetu wa Jimbo la Lupembe hawanielewi ni kwa nini barabara hii kandarasi haitangazwi wakati imesanifiwa muda mrefu na tayari ilitakiwa iwe imeshaanza kutengenezwa muda mrefu. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri ashughulikie suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna barabara moja ya Ilunda – Igongolo – Kivitu - Ilengititu – Kifumbe. Barabara hii inasimamiwa na TANROADS, lakini imekuwa ikitengenezwa kilometa tisa tu, imeishia sehemu fulani njiani, kule mbele haiendelei kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana TANROADS waongeze kipande kile kingine kwa maana waende Kijiji cha Kivitu kutoka Idonda, Igongoro waende Kivitu baadaye iende Ilengititu na itokeze kule Kifumbe ambako ni Jimbo la Makambako ili angalau tuweze kutengeneza mtandao mzuri wa barabara na hatimaye mazao ya eneo lile yaweze kusafirishwa kirahisi zaidi hasa wakati wa mvua. Kama nilivyosema Jimbo langu mimi linapata kipindi kirefu sana cha mvua, miezi nane mvua inanyesha, kwa hiyo inapofikia wakati wa kuvuna mazao haya hayawezi kufikia soko kwa urahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia kuhusu minara ya simu kwa maana ya mawasiliano. Kuna kata kama tano hivi simu hazishiki vizuri hasa Kata zile za Ninga, Ikondo, Mfiga lakini pia na maeneo mengine ya vijijini ambako simu hazishiki vizuri. Nilishapeleka taarifa na nashukuru kwamba Waziri aliniahidi kwamba mwaka huu wa fedha watapeleka minara katika maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana tujitahidi ili tuweze kufungua mawasiliano na hatimaye waweze kufanya biashara na shughuli zao za kiuchumi vizuri. Maana biashara za kilimo ni lazima uwe na mawasiliano ya karibu sana na soko. Kama hakuna mawasiliano ni vigumu sana kujua ni wapi bidhaa yako uweze kuipeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukiwafungulia mawasiliano na tukawa tumetengeneza barabara hizi kama nilivyosema hasa barabara kuu hii ya Kibena – Lupembe – Madeke – Mlimba - Morogoro, kasi ya uchumi itakua na hatimaye maisha ya Watanzania yataboreshwa kwa sababu uzalishaji utakuwa umeongezeka na bidhaa zao zitazalishwa kirahisi zaidi kwa sababu barabara ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nirudie kuipongeza Serikali, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa jitihada anazozifanya kuhakikisha kwamba anafungua mawasiliano katika nchi hii. Niwapongeze Mawaziri wote kwa maana ya Waziri Profesa Mbarawa na Naibu Mawaziri Mheshimiwa Nditiye na Mheshimiwa Kwandikwa. Pia nimpongeze Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa ambayo wanafanya. Niombe sana Mwenyezi Mungu awabariki ili waendelee kuwa na afya njema na hatimaye waweze kutuletea sisi Watanzania maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa nafasi na mimi niweze kupata kuchangia kwenye Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuanzisha utaratibu wa elimu bila malipo, nimpongeze sana kwa Wizara ya Elimu pia kwa kazi ambazo wanazifanya kwa maana ya Waziri, Naibu Waziri na Katibu wa Wizara hii na Makamishna wote na watengaji wote wa Wizara kwa kazi kubwa ambazo wanazifanya ili kuhakikisha kwamba Watanzania wanaweza kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu wameeleza sana Waheshimiwa Wabunge na wameeleza vizuri sana kuhusu elimu kushuka. Mimi niseme kwamba hili suala halihitaji kuangalia upande mmoja, ni lazima Serikali, wazazi na wadau wote tuweze kushirikiana kuhakikisha kwamba ni namna gani tutaboresha elimu yetu. Mheshimiwa Rais ameweka elimu bure ili kutoa fursa kuhakikihs kwamba watanzania wote wanapata fursa ya kupata elimu ya msingi na sekondari. Kwa hiyo sasa kwa kuwa tayari Rais ameshafungua fursa sasa ni jukumu letu sisi wadau, wana taaluma, pia ni jukumu letu sisi Wabunge kuwaelimisha wazazi namna gani ya kuweza kushirikiana na walimu kwenye mashule ili elimu yetu iweze kuboreshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tukibaki tunalaumiana hivi hatutaweza kufanikiwa, lazima sisi sote tushiriki katika kuhakikisha kwamba elimu yetu kwenye majimbo yetu na kwenye maeneo yetu inaboreshwa. Kwa hiyo, jitihada za kuboresha elimu zinaanza na wewe Mbunge zinaanza na wazazi waliopo katika maneo husika lakini pia kwa kushirikiana na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme juu ya elimu hii ya ufundi. Tunaenda kwenye Tanzania ya viwanda ni lazima kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge wengine, ni lazima tuwaandae vijana wetu. Mimi nafikiri kama alivyoeleza Mheshimiwa Mwalongo alieleza vizuri sana katika mchango wake aliutoa juzi kwamba ni muhimu tuwe na masomo ya ufundi kwenye shule zetu za sekondari, lakini mimi niseme kwamba ni vizuri tuanze mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kwenye kila shule ya msingi ikiwezekana tuwe na darasa la ufundi, wanafunzi wanapokuwa kwenye shule ya msingi wapate stadi za ufundi pale pale shuleni, kama ilivyokuwa zamani. Tulivyokuwa tunasoma shule ya msingi tulikuwa tunajifunza mambo mbalimbali. Kuna shule nyingine tulikuwa tunajifunza useremala, kuna shule nyingine wanajifunza utengenezaji wa vitu mbalimbali na hatimaye tukapata mafundi wengi, mafundi wengi wanaojenga nyumba sasa hivi huko vijijini na maeneo mengine, mafundi wengi wanaofanya kazi za welding yaani uungaji wa vyuma, mafundi wengi wanaofanya kazi za umeme wamejifunza wengine toka shule za msingi na wengine wamejifunza sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tukiamua kwamba shule zetu za msingi ziwe na angalau wanafunzi wawe wanapata kipind kimoja cha ufundi, nina hakika kabisa tutapata vijana wengie, tutapata mafundi michundo wengi. Kwa hiyo, mimi nitoe rai kwa Serikali, niiombe tubadilishe sera kidogo tuanzishe shule za misingi kule kule angalau kuwe na kipindi cha ufundi toka shule ya msingi, akienda sekondari akutane na darasa la ufundi na hatimaye wengine pengine waweze kwenda kwenye vyuo vingine huko juu. Kwa hiyo, watoto tukiwaanzisha mapema watapenda ufundi na watapenda kusoma masomo hata ya sayansi ili waje kuwa mafundi mazuri baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haiwezekani kuanzisha kwenye shule zote basi angalau kwenye kata tuchague shule moja ambayo itakuwa ni shule ya msingi ya ufundi ili watoto waweze kujifunza pale, na ikiwezekana hata wale wengine wanaokaa maeneo yanayozunguka ile shule wanaweza wakaenda kujifunza elimu ya ufundi pale kwenye ile shule ya ufundi katika kata zetu. Kwa hiyo, tukianzisha utaratibu huu tutawezesha vijana wetu wengi kwanza kuwa na uwezo wa kujiajiri kwa sababu amejifunza ufundi fulani. Kwa hiyo, niombe sana Wizara tujaribu kuchukua mawazo haya ili tuweze kusaidia ili vijana wetu wengi waweze kuenenda na uchumi wa kati, uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeongea sana juu ya suala la lugha ya kufundishia. Imekuwa ni mjadala wa muda mrefu sana. Tumekuwa tukijadili kwamba either tuamue twende kwenye kiingereza au twende kwene kiswahili, na muda mwingi tumekuwa tukifundisha shule za msingi kwa kiswahili lakini wanafunzi hawa wakienda sekondari wanakutana na lugha ya kiingereza. Hii imekuwa ikileta confusion kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia watoto wa sekondari walio wengi hawaielewi lugha ya kiingereza na wengine wakiwa wanajibu mitihani wanaandika kwa kiswahili; na kwa kuwa wameandika jibu ambalo sio lugha rasmi, wametumia lugha isiyo rasmi wamekuwa wakikatwa kwa maana wakipata kosa kwenye yale majibu yao. Kwa hiyo kumbe Watanzania wengi wanaelewa kiswahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ni kwanini tusiamue sasa tukaanza darasa la kwanza mpaka Chuo Kikuu tukafundisha kwa kiswahili?

Mheshimiwa Mwneyekiti, wengine wamesema kwamba tutakuwa tumejifungia, hapana! Mbona nchi hizi zilizoendelea, tumeona China, tumeona Korea wanafundisha kwa lugha yao ya Kikorea lakini ndiyo nchi ambazo tunasema leo kwmaba zinakuwa uchumi kwa kasi kubwa sana. Na sisi tuamue, tusibakie tu kwenye kiingereza, tusibakie tu kwenye hii lugha ya wakoloni, turudi kwenye kiswahili. Tuanze kufundisha kiswahili toka darasa la kwanza, sekondari na hatimaye Chuo Kikuu, naamini Watanzania kwa sababu ni lugha mama wataelewa vizuri na wataweza kujibu majibu kwenye mithani vizuri na ufaulu utapanda kwa kuwa wanatumia lugha ambayo wao wenyewe wanaielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia juu ya Kitengo cha Udhibiti Ubora. Kitengo hiki cha Udhibiti Ubora kipo hoi, hawana magari, hawana fedha za kujaza mafuta kwenda kukagua shule na tumesema kwamba Udhibiti wa Ubora ndilo jicho la Serikali, ndilo jicho tunalolitumia kuangalia nini kinachoendelea kwenye shule zetu. Niiombe sana Serikali iwezeshe kitengo cha udhibiti ubora waweze kupata magari lakini pia waweze kupata fedha za kuweza kujaza mafuta na kwenda kukagua kwenye sule zetu hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ilivyo, kama Halmashauri haina fedha, wadhibiti ubora hawawezi kwenda kwenye shule, hawana uwezo wa kwenda kwenye shule kufanya ukaguzi…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza sana Mawaziri wote, Mheshimiwa Profesa Ndalichako, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, na Naibu Waziri Mheshimiwa Ole Nasha, kwa usimamizi mzuri wa Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ndiyo msingi muhimu sana wa maendeleo ya mwanadamu na uchumi wa nchi yetu ya Tanzania. Pamoja na changamoto nyingi tunazopitia kama nchi, nimpongeze sana Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuanzisha utaratibu wa kutoa elimu bila malipo kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne. Hii inasaidia Watanzania wanyonge nchini kupata fursa ya kupata haki yao ya msingi yaani elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya nchi yetu sasa ni kujenga uchumi wa viwanda. Ili kufikia uchumi huo wa viwanda ni lazima sekta ya elimu iwaandae vijana wetu mashuleni kupata elimu ya ufundi yaani stadi au ujuzi mbalimbali. Ili kufikia azimio hilo nashauri Serikali yetu ianzishe utaratibu wa kuwa na somo la ufundi kuanzia shule ya msingi. Kila shule ya msingi na sekondari angalau kuwe na darasa, angalau kipindi kimoja ambapo watoto wetu walioko shule za msingi watajifunza stadi mbalimbali kama vile uashi, useremela, ushonaji, uhunzi au uungaji vyuma, umeme na kadhalika. Hii itasaidia watoto kupenda masomo ya ufundi na baadae kupata fursa ya ajira kwenye viwanda vidogo vidogo na vikubwa hata kujiajiri wenyewe. Katika kufanikisha jambo hili, tunaweza tukachagua shule moja ya msingi katika Kata na tukaanzisha darasa hilo la ufundi.

Mheshmiwa Mwenyekiti, lugha ya kufundishia na kujifunzia. Tumekuwa na mjadala kwa miaka mingi nchini juu ya lugha ipi itumike kwa kufundishia na kujifunzia kwa wanafunzi wetu. Historia ya nchi nyingi ambazo uchumi wake umekua kwa haraka sana katika miongo hii ya karibuni ni kutokana na kuongezeka kwa ubora wa elimu. Ubora wa elimu unatokana na kutumia lugha inayoeleweka kwa wanafunzi na walimu wanaowawezesha wanafunzi kujifunza. Mfano, nchi za China, Korea, Malaysia na kadhalika. Watanzania tunapozaliwa tunaanza kujifunza lugha za kienyeji (mother tongue) tukiingia darasa la kwanza tunakutana na lugha ya kiswahili na tunatumia kujifunza kwa miaka saba. Baada ya miaka saba, Mtanzania akienda sekondari anakutana na lugha mpya ya kiingereza. Matokeo ya mchanganyiko huo, wanafunzi wetu wanakuwa wakishindwa kumudu masomo ya sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, kwenye mitihani ya Taifa ya kidato cha pili na nne, watoto wamekuwa wakiandika kwa lugha ya kiswahili katika kujibu maswali. Mtahiniwa anaweza akawa anajua kabisa hoja anayotakiwa kuieleza au kujibu, lakini kwa kuwa ameelewa kwa kiswahili wamekuwa wakishindwa kuandika kwa lugha ya kiingereza na badala yake anaandika kiswahili na kukosa alama kwa kuwa anatumia lugha isiyo rasmi kwenye somo husika. Hivyo nashauri ni muhimu Serikali iamue tufundishe masomo yote kwa kutumia lugha ya kiswahili ambayo ndiyo lugha mama na inaeleweka kwa Watanzania wote. Lakini kama tunadhani kiingereza ndiyo lugha bora zaidi, basi tufundishe kiingereza toka chekechea mpaka chuo kikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu udhibiti ubora wa elimu nchini; kitengo hiki ni muhimu sana katika kuangalia au kusimamia ufundishaji na ujifunzanji wa wanafunzi. Idara ya ukaguzi pamoja na umuhimu wake, lakini inakabiliwa na matatizo makubwa mawili, uhaba wa magari na kukosa fedha za kununulia mafuta ili waweze kuzifikia shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule zinakaa miaka mitatu mpaka minne bila kukaguliwa. Hii ni hatari kubwa sana kwa maendeleo ya elimu katika nchi yetu. Wizara ya Elimu ione umuhimu wa kuwawezesha wadhibiti ubora kufika mara kwa mara kwenye shule zetu ili kufanya ukaguzi na kujua kama walimu wanafuata miongozo vizuri, pia mikakati na njia za kufundishia zinatumika vizuri. Hii itasadia walimu kufundisha vizuri na kuwafanya walimu wawe mahiri katika masomo yao. Hili litaongeza ufaulu wa wanafunzi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu, naipongeza Serikali kwa kuongeza idadi ya wanafunzi wanaonufaika na mikopo hiyo. Pamoja na ongezeko hilo bado Wizara hasa Bodi ya Mikopo iwe makini katika kufanya tathmini ya wanafunzi wenye sifa ya kupata mikopo. Kuna baadhi ya watoto wanaotoka kwenye familia maskini wanakosa mikopo. Kigezo cha kwamba kipaumbele ni wale waliosoma shule za Serikali ndiyo hawana uwezo siyo sahihi sana, kuna watoto wamekuwa wakisomeshwa na Waheshimiwa Wabunge, Makanisa na watu wengine wasamaria wema baada ya kuona wazazi wao hawana uwezo au yatima, lakini wanapohitimu masomo yao na kuingia Chuo Kikuu hukosa mkopo kwa kuwa wamesoma shule zisizo za Serikali. Hivyo naomba sana Serikali itathmini kwa makini juu ya vigezo vya kupata mikopo kwa wanafunzi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kazi kubwa wanayoifanya kwa ajili ya kumtua mama ndoo kichwani. Nampongeza Waziri wa Maji na Umwagiliaji kwa kazi kubwa anayoifanya akishirikiana na Naibu Waziri. Kwa kweli Mheshimiwa Kamwelwe (Waziri) na Mheshimiwa Aweso wamepewa Wizara stahiki na wanaitendea vema Wizara hii, ni imani yangu kuwa ifikapo mwaka 2020, vijiji vingine na mitaa mingi nchini itafikiwa na huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai lakini pia maji ni maendeleo. Shughuli zote za kibinadamu na uhai wetu unategemea sana uwepo wa maji. Akinamama nchini wanatumia muda mwingi kutafuta maji kwa ajili ya kupika na matumizi mengine ya nyumbani. Wanafunzi mashuleni wamekuwa wakipoteza muda mwingi kutafuta maji na hii imekuwa ikiathiri taaluma. Kwa kuwa tulishakuwa na shilingi 50 kwenye kila lita ya mafuta na matokeo yake tumeyaona, bajeti ya maji imekuwa ikiongezeka na miradi ya maji mjini na vijijini ikiongezeka pia. Hivyo napendekeza tuongelee tozo toka shilingi 50 kwenda shilingi 100 ili bajeti iweze kuongezeka. Naamini tukiongeza shilingi 50 tena vijiji vingi na mitaa mingi itapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania ni nchi yenye baraka au imebarikiwa sana, tunapata mvua nyingi sana ambazo zimekuwa zikisababisha mafuriko na uharibifu mkubwa wa miundombinu na majengo. Kuna baadhi ya nchi, mvua nyingi ni fursa za kimaendeleo. Nashauri maeneo yenye mvua nyingi ufanyike utaratibu wa kuvuna maji haya ili yatumike wakati wa kiangazi. Maeneo kama Mkoa wa Dodoma, Singida, Tabora, ungeanzishwa mradi wa uvunaji wa maji ya mvua na ujenzi wa mabwawa makubwa kwenye mabonde kama ya Fufu na mabonde mengine. Maji haya yakivunwa yanaweza kutumika kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji au matumizi ya nyumbani wakakti wa ukame.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Lupembe Halmashauri ya Wilaya ya Njombe imekuwa ikipata fedha kidogo sana kwa ajili ya miradi ya maji ukilinganisha na Halmashauri nyingine nchini. Vijiji vingi vya Halmashauri ya Wilaya ya Njombe Vijijini haina maji ya bomba pamoja kuwa na vyanzo vingi vya maji. Mfano Vijiji vya Matiganyoro, Myombo, Kichiwa, Upani, Ilengititu, Taganende, Kivitu, Lima, Isitu, Havaiga, Isohivaye, Kanikelele, Igombole, Ikang’asi, Welela, Sovi na Iyembela. Lakini naishukuru Serikali kwa kutenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, naamini fedha hizi zikitoka zitapunguza kero kubwa ya maji katika Jimbo la Lupembe na Halmashauri ya Wilaya ya Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo kubwa la usimamizi wa miradi ya maji. Wakandarasi wengi wamekuwa wakitengeneza miradi hii chini ya kiwango na kwa kutumia gharama kubwa. Ni muhimu Wizara hasa Waziri wa Maji na wataalam wa Wizara kuwa jirani na miradi hii, kuwa na ufuatiliaji wa mara kwa mara ili kusitokee ubadhirifu unaofanywa na baadhi ya kandarasi wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia kumpongeza Mheshimiwa Rais, Waziri wa Maji, Naibu Waziri na wataalam wa Wizara ya Maji kwa kusimamia na kufuatilia miradi ya maji. Hii itatusaidia kukua kwa uchumi wetu kwa kasi kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja iliyopo mezani.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kidogo kwenye Wizara ya Mipango na Fedha kwa maana ya bajeti nzima kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa namna anavyofanya kazi, nimpongeze pia Naibu Waziri namna wanavyofanya kazi nzuri ya kuhakikisha kwamba Watanzania mipango ya fedha na mipango mingine inaenda vizuri; niwapongeze wanakwenda vizuri. Nimwombe Mwenyezi Mungu aendelee kuwajalia afya njema ili wasikate tamaa wasirudi nyuma, waweze kwenda mbele na kutusaidia kuhakikisha kwamba rasilimali za nchi hii zinawekwa vizuri na hatimaye zinagawanywa vizuri kwa Watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, nianze kusema kwamba wananchi Watanzania walio wengi wamejiajiri kwenye shughuli za kilimo, takribani asilimia 65.5 wanajihusisha na kilimo. Kwa hiyo tafsiri yake ni kwamba uchumi pengine wa nchi ya Tanzania unategemea sana kilimo. Kwa hiyo ni lazima tujikite tuhakikishe kwamba tunaboresha sekta ya kilimo ili tuweze kupata pato la Taifa na liweze kukua kutokana na shughuli za kilimo.

Mheshimiwa Spika, shughuli za kilimo haziwezi kukua kama hatujaweka miundombinu mizuri wezeshi; na moja ya miundombinu wezeshi mizuri ambayo inaweza ikasababisha kilimo kiweze kukua na hatimaye pato la Taifa liweze kukua ni barabara. Sote tunatambua kwamba kilimo kinafanyika maeneo ya vijijini na huko ndiko wakulima wetu waliko, wanazalisha kwa kiasi kikubwa, lakini changamoto kubwa imekuwa ni barabara. Imekuwa hawawezi kufikisha mazao kwa wakati, mazao hayawezi kufikia soko kwa wakati na hata yakifika yanakuwa tayari yameshapoteza ule ubora wake.

Mheshimiwa Spika, juzi wiki iliyopita tulikuwa kwenye mkoa wetu, Mkoa wa Njombe na Kamati ya Kilimo. Kamati ilijionea yenyewe namna jinsi wakulima wetu wanavyopoteza fedha nyingi, rasilimali nyingi kutokana na changamoto kubwa sana ya barabara. Njombe tunazalisha mazao mengi; tunazalisha chai, tunazalisha matunda, tunazalisha mbao, tunazalisha kila aina ya mazao ambayo yanazalishwa hapa nchini, lakini changamoto kubwa ukiangalia mazao yote kwa ujumla wake kwa hali ya hewa ya Njombe ni hali ya mvua. Kwa hiyo yamekuwa yakiathiriwa sana na barabara zetu ambazo si nzuri sana, kwamba hazipitiki wakati wa kifuku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme juu ya zao mojawapo zao la Parachichi. Zao la parachichi katika nchi hii linalozalishwa Njombe ni la tofauti sana. Ni wakati ambapo Njombe peke yake inazalisha hili zao, maeneo mengine duniani kunakuwa hakuna uzalishaji wa parachichi. Sote tunajua matumizi makubwa ya parachichi katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali ikiwemo mafuta, mafuta ya nywele, dawa mbalimbali, lakini ukiangalia miundombinu ambako hili zao linazalishwa ni mibovu sana.

Mheshimiwa Spika, niombe kwenye upande hasa wa barabara, tukiangalia barabara zetu hasa kwa mfano, kwenye jimbo langu Jimbo la Lupembe, barabara ya kutoka Kibena kwenda Lupembe mpaka Madeke ambako huko kuna uzalishaji mkubwa sana wa parachichi, barabara hii imekuwa haipitiki wakati wa kifuku.

Mheshimiwa Spika, katika Bunge hili tumepitisha bajeti mara kadhaa, tumepitisha bajeti ya mwaka 2016/2017, tumepitisha tumeweka fedha. Tumepitisha bajeti ya mwaka 2017/2018 na hata mwaka huu 2018/2019, tumeweka fedha pale. Fedha hizi zimekuwa hazitoki, kwa hiyo kimsingi tunapoteza fedha nyingi kwa kuacha yale mazao yaliyopo kule vijijini yasiweze kutoka kwenda kwenye lami, kwenda kwenye soko kwa sababu ya ubovu wa barabara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimwombe ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mpango lakini pia niombe kwa Serikali yetu kwa ujumla, niombe kwenye bajeti hii ya mwaka huu tujitahidi basi barabara ya Lupembe kwa maana ya Kibena – Lupembe- Madeke na kuunganisha kwenda Morogoro iweze kupewa fedha ianze kujengwa kwa kiwango cha lami ili mazao haya niliyotaja kama chai na parachichi yaweze kusafirishwa kirahisi zaidi na yaweze kufikia soko.

Mheshimiwa Spika, naamini kabisa tukizalisha kwa wingi, tukiweka barabara zikawa zinapitika kipindi chote cha mwaka mazao kama chai, parachichi kama nilivyosema, mbao na nguzo za umeme zitaweza kupitishwa kwenye barabara hii na hatimaye tutaokoa fedha nyingi sana ambazo tumekuwa tukipoteza wakati wa mvua kutokana na ukosefu wa barabara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Mpango kwa kushirikiana na Serikali nzima na Wizara zote tuhakikishe hii barabara inatengenezwa kwa kiwango cha lami na barabara nyingine zilizopo katika Mkoa wa Njombe ambako kama nilivyosema kuna uzalishaji mkubwa sana wa parachichi ambazo zinazalishwa Njombe tu.

Mheshimiwa Spika, katika dunia nzima kuna msimu ambako Njombe tu zinapatikana na wafanyabiashara wote duniani wanakuja kununua parachichi Njombe ili ziweze kwenda kwenye masoko hayo na tuweze kupata mabilioni ya fedha mengi na hatimaye kukuza pato la Taifa, tuhakikishe kwamba barabara hizi zinatengenezwa kwa kiwango ili ziweze kutumika wakati wa kifuku.

Mheshimiwa Spika, pia niseme jambo moja juu ya risiti za EFD hasa kwa wazalishaji wa mazao ya misitu hasa mbao. Kumekuwa kuna tatizo Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa wakulima wangu wa Lupembe wanaozalisha mbao. Zinapokwenda sokoni njiani wanakutana na kikwazo kwamba ni lazima aliyeuza hiyo miti, aliyezalisha hiyo mbao lazima awe ana risiti ya EFD. Sasa mkulima ameuza miti yake ameuza heka mbili, heka tatu, heka tano tu unamwambia awe na risiti ya EFD na anauza pengine kwa miaka 15 mara moja tu; sasa hii mashine ya EFD atapata wapi?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe Wizara ya Fedha wajaribu kuliangalia jambo hili hasa la EFD mashine kwenye mbao zinazotokana na wakulima wa misitu, hasa wakulima wa misitu ya mbao. Kwa hiyo niombe tuliangalie vizuri.

Mheshimiwa Spika, pia nataka niseme kidogo juu ya jambo moja la vifungashio. Tulipita na Kamati ya Kilimo na Uvuvi, kuna maeneo ambako tayari kuna wafanyabiashara wananunua mazao haya, kama nilivyosema matunda na mazao mengine kama njegere na mazao mengine. Wanatumia vifungashio kutoka Kenya na pale nje wanaandika Made in Kenya. Kwa hiyo, inaonekana kwamba zao lile au njegere hizo au parachichi hizo zimezalishwa Kenya wakati zimezalishwa Lupembe au zimezalishwa pale Njombe. Kwa hiyo niombe wajaribu kudhibiti hasa hawa wanaochukua mazao yetu haya wafungashie vifungashio ambavyo vitaandikwa kwamba hilo zao au hiyo bidhaa aliyozalisha imezalishwa sehemu fulani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo itajwe sehemu ambako bidhaa hiyo imezalishwa, lakini siyo itajwe eneo lingine kwa mfano wanaandika Made in Kenya na mwisho wa siku inaonekana Kenya ndiyo inayozalisha hayo mazao kumbe tunazalisha hapa Tanzania, tunazalisha Njombe. Kwa hiyo niombe wajaribu kufuatilia hili na kulidhibiti kwenye upande wa vifungashio ili vioneshe sehemu ambako zao hili limezalishwa na hasa kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine niseme juu ya kodi ya mapato hasa kwa wazee wastaafu ambao wamefungua vibiashara vidogo vidogo. Wazee hawa wamekuwa wakipata zile pensheni zao wanafungua biashara ndogo, anakuwa na biashara ya milioni tatu, nne, tano halafu tunakwenda kuwadai kodi. Hebu tuangalie hawa wazee wamefanya kazi miaka mingi sana, wametusaidia sana, tuangalie kama biashara ndogo hizi angalau tuwaachie ili waweze kujiwezesha waweze kujikwamua kwenye maisha yao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nikushukuru sana, naamini Wizara itayachukulia kimakini haya mambo na niunge mkono hoja kwa asilimia mia hoja hii iliyopo mbele yetu. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika Wizara hizi mbili TAMISEMI na Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa shughuli anazozifanya za kuhakikisha kwamba anatetea maisha ya Watanzania na kuleta maendeleo katika nchi yetu. Pia kwa namna ya pekee nichukue fursa hii nimshukuru sana kwani katika jimbo langu aliweza kutoa vitanda 25 , vitanda 20 vikiwa ni kwa ajili ya wagonjwa wa kawaida na vitanda vitano kwa ajili ya labour, nashukuru sana .

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri Suleiman Jafo kwa jinsi anavyojituma katika kuhakikisha kwamba anaisimamia vizuri Wizara yake ya TAMISEMI. Vile vile nimpongeze Mheshimiwa Mkuchika pia naye anajitahidi kusimamia kuhakikisha kwamba mambo yanakwenda vizuri. Niwapongeze pia Naibu Mawaziri wote Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Kandege; niwapongeze Katibu Mkuu injinia Musa Iyombe, niwapongeze Naibu Makatibu Wakuu kwa namna wanavyofanya kazi usiku na mchana kuhakikisha kwamba wanawaletea maendeleo Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi wanazofanya Wizara hizi zote mbili ni kazi zinagusa maisha ya Watanzania, zinagusa maendeleo ya wananchi. Maana sote tunajua kwamba Wizara hizi hasa Wizara ya TAMISEMI inahusika sana na huduma za jamii kama vile ujenzi wa shule, vituo vya afya, ujenzi wa barabara na hakuna eneo ambalo shughuli hizi hazifanyiki, kila kijiji na kila eneo kama ni mjini na vijijini kote shughuli hizi zinaendelea. Kwa hiyo wanafanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha kwamba Watanzania wanyonge wanapata maendeleo, kwa hiyo nawapongeza wote kwa maana ya mawaziri lakini pia na watumishi wote wa Wizara zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kazi wanazofanya zinagusa maisha ya watu, niombe sana Mwenyezi Mungu awasaidie ili kuhakikisha kwamba wanasimamia vizuri hasa recourses. Pesa wanayoiomba ni trilioni 6.58, ni fedha nyingi lakini ndogo kutokana na jinsi matatizo yaliyopo huko kwenye maeneo yetu yalivyo mengi, kwa hiyo niwaombe sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana hasa kwenye zile fedha za maendeleo hasa zile zinazotokana na wafadhili, tujitahdi kusimamia vizuri kwa sababu tusipozisimamia vizuri zinaweza zikasababisha manung’uniko katika baadhi ya maeneo. Halmashauri yetu sisi ya Wilaya ya Njombe ipo Mkoa wa Njombe na ni Halmashauri mama ya Mkoa. Mkoa wa Njombe una halmashauri sita na Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ndiyo iliyozaa halmashauri hizi zote; na sasa hivi resources zake zote zimekuwa zikigawanywa kwenye halmashauri nyingine na imebaki halmashauri mzee ambaye hana kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halmashauri hii pamoja ni kwamba ni halamashauri mama ni halmashauri pekee ambayo haina hospitali ya wilaya, halmashauri zote tano za Mkoa wa Njombe zina hospitali za wilaya lakini Halmashauri hii ya Wilaya ya Njombe haina hospitali hata moja ya Serikali lakini pia hata ya binafsi hatuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna vituo vya afya vinne tu; tuna Vituo vya Lupembe, Matembwe, Kichiwa na Sovi. Vituo hivi vyote vilikuwa havina huduma ya upasuaji. Mpaka mwaka 2015 tulikuwa na kituo hicho kimoja cha Lupembe tukaongeza vikawa baadaye vinne na sasa hivi tunajenga kituo kingine cha pale Ikuna ambacho tupo kwenye umaliziaji (finishing), kwa hiyo si muda mrefu tutakuwa pengine na vituo vitano vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka 2016 nilivyoingia Bungeni hapa, nimekuwa nikiomba Kituo cha Afya cha Lupembe kipewe fedha kwa ajili ya kujenga theater, kutoa huduma ya theater na kujenga wodi. Kituo hiki ni cha muda mrefu sana, mwaka 1985 ndipo kilipoanza kazi yake, kwa hiyo ni kituo ambacho kimeshachakaa. Hata hivyo, bahati mbaya hatujapata hizo fedha pamoja na kwamba tulikuwa tumeahidiwa muda mrefu, lakini hatujapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, basi kwa kuwa na sisi tulianza kujipanga kuhakikisha kwamba wananchi wetu wale wanapata huduma ya upasuaji, baada ya kuona akinamama wanafariki wanafia njiani kwa kukosa huduma ya uzazi. Kwa hiyo kwa uchungu huo tukaamua kujipanga na mimi Mbunge kwa kushirikiana na halmashauri tukajenga jengo la mama na mtoto. Mimi nilichangia bati katika lile jengo kwenye fedha binafsi nje ya Mfuko wa Jimbo na halmashauri imesaidia wananchi wamefyatua tofali na tukajenga lile jengo ambalo Mheshimiwa Kigwangalla alikuja na akalaifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla alipokuja tulimwomba fedha kwamba tupate angalau fedha kidogo kwa ajili ya huduma hii ya upasuaji lakini mpaka leo hatujapata. Hata Kituo kingine kila cha Kichiwa tuliomba tupate fedha na wananchi wameshafyatua tofali tayari, lakini mpaka leo hii hatujapata fedha yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi mwezi wa Pili tumeambiwa kwamba tukae kikao kuna fedha milioni mia sita zitakuja, tukakaa vikao vyote Kamati zikakaa kwenye halmashauri yangu na Baraza la Madiwani likakaa, tumetuma Mkurugenzi na Mwenyekiti wamekuja hapa lakini wamerudi bila fedha. Nitaomba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI atakaposimama basi tuweze kupata ufafanuzi angalau wa hizi fedha milioni mia sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru kwa namna ya pekee Mheshimiwa Jafo, katika bajeti tumeona kuna hospitali ya wilaya itaaanza kujengwa na wametutengea shilingi bilioni 1.5 nashukuru sana. Hata hivyo pamoja na kutenga hizi fedha tunaomba hizi fedha kwenye hivi vituo ili tuweze kujenga chumba cha theater room na vyumba vingine vinavyohitajika ili hatimaye wananchi wetu hawa wasiendelee kufa kwa sababu ya kutekeleza jukumu lao la msingi la kuongeza wanadamu hapa duniani, kwa hiyo namwomba sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme juu ya barabara kwa maana ya TARURA. TARURA kwangu wanafanya kazi nzuri sana lakini wanakwamishwa na fedha, bado fedha haziendi za kutosha. Sisi kwenye halmashauri yetu tuna mtandao wa barabara ambao una kilometa 586 na zaidi, lakini fedha kwenye bajeti mwaka jana tulipangiwa biloni 1.1, tukapata miloni mia saba na milioni mia nne zimeenda kulipa madeni ya mwaka wa fedha ulioisha, kwa hiyo tumebakiwa na milioni mia tatu. Sasa ukiangalia mtandao wa barabara ulivyo na kiasi cha fedha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuunga mkono hoja. Ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia huu mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kuipongeza Serikali, kumpongeza Mheshimiwa Rais mwenyewe kwa namna anavyofanya, kwa namna alivyoanza kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Wamesema hapa kwamba tayari Rais ameweza kuhakikisha kwamba mipango ya ununuzi wa ndege imekamilika na inaendelea vizuri, barabara za lami zinaendelea kutengenezwa lakini pia reli inaendelea kujengwa, reli ya kisasa kabisa ambayo ni standard gauge, lakini pia ujenzi wa meli katika maziwa makubwa nao unaendelea na mipango mingine mingi mizuri inaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa namna anavyoisimamia vizuri hii Wizara ya Fedha na Mipango, kweli anaitendea haki anaisimamia vizuri sana. Nimpongeze pia Naibu Waziri wake, anafanya kazi nzuri, tuombe Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki waendelee kufanya kazi na hatimaye sisi Watanzania tuweze kupata maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nichangie kidogo kwenye kilimo; Sekta ya Kilimo kwa sehemu kubwa Tanzania ndiyo inayotegemewa zaidi. Zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania wanajihusisha na kilimo cha mazao mbalimbali, lakini pia kuna zao hili la mahindi ambalo sehemu kubwa, karibu nchi nzima tunalima, lakini pia mikoa sita ya Nyanda za Juu Kusini; Mbeya, Rukwa, Katavi, Ruvuma, Songwe na Njombe ndiyo wanaolima sana haya mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ukienda kwenye mikoa hii mahindi ya mwaka jana yamejaa kwenye nyumba na mwaka huu yamejaa, wakulima hawajui wafanye nini na wakati huo huo msimu wa kilimo umeshaanza lakini hawajauza mazao yale na mbolea inauzwa bei juu, kwa hiyo sasa hatujui namna gani Serikali itatusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niombe Serikali, ili tusiweze kuwa na hali kama hii huko mbeleni tujitahidi kuwa na kitengo maalum ambacho kitahusika sanasana na utafiti wa masoko ya mazao yote ya kilimo kwa maana ya mazao ya biashara na yale ya chakula, kuwe na kitengo hicho ambacho kitazunguka nchi nzima na kufanya utafiti ni wapi zao lipi litauzwa ili tuondoe hii adha kubwa ambayo wakulima wanalima halafu mwisho wa siku haya mazao yanabaki bila kupata soko na mwisho wa siku inakuwa ni hasara kubwa kwa wakulima na pato la Taifa linapungua kwa sababu tunakuwa tumezalisha kitu ambacho hakiwezi kuuzwa kinabaki tu kwa ajili ya chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana hiki kitengo kitatusaidia kuhakikisha kwamba mazao yote yanapata masoko huko duniani kwa sababu sasa hivi tuna masoko pale DRC, wanahitaji mahindi, Kenya wanahitaji mahindi, sasa sijajua kuna tatizo gani kwa nini mahindi hayaendi huko DRC au hapo Kenya ambapo wana shida ya chakula. Kwa hiyo, tufanye hivyo, tuanzishe kitengo maalum ambacho kitafanya utafiti wa masoko hasa masoko haya ya mazao ambayo tunazalisha hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo lingine juu ya Mradi wa Mchuchuma na Liganga, ule wa makaa ya mawe na chuma. Huu mradi ni wa muda mrefu na umesemwa muda mrefu sana kwenye vitabu toka mwaka 2016 tulivyoingia Bungeni lakini mpaka sasa bado haujaanza, taarifa zinaonesha kwamba bado mazungumzo yanaendelea. Sasa tunaomba kujua ni lini mazungumzo haya yataisha? Kwa sababu huu mradi ni muhimu; kwanza unakwenda kuzalisha chuma ambacho kitasaidia kutoa raw material kwenye viwanda vyetu. Lakini pili utazalisha umeme ambao utasaidia sasa, utawezesha hata viwanda vidogo vidogo viweze kufunguliwa kwa sababu kutakuwa kunawaka umeme na utakuwa wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe Serikali mchakato huu wa mazungumzo ni vizuri uwahi basi ili angalau huu Mradi mkubwa wa Mchuchuma wa makaa ya mawe na chuma uweze kuanza ili mwisho wa siku tuweze kupata faida hizo na pia tufungue fursa za vijana kupata ajira kwenye maeneo hayo ambako chuma kitazalishwa, lakini pia kutakuwa na makaa ya mawe, lakini kwa maeneo hayo pia na viwanda vingi vitaongezeka kwa sababu tuna raw material sisi wenyewe lakini pia tuna umeme wa kutosha nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme juu ya uvuvi, niipongeze Serikali, imeendelea vizuri lakini pia nipongeze Wizara inaendelea kudhibiti uvuvi haramu, nawapongeza sana mnafanya kazi kubwa maana tukiacha samaki wakapotea itakuwa ni mbaya, lazima tuwe na samaki waendelee kuzaliana na tuendelee kuuza na nipongeze kwamba tayari Serikali imeanza mpango wa kujenga bandari ya uvuvi, nipongeze sana, tunataka twende kwenye uvuvi, siyo tu ule wa mwaloni, siyo tu ule uvuvi wa territorial, twende sasa kwenye uvuvi wa ndani, twende kwenye EEZ, kwenye Exclusive Economic Zone, ndivyo nchi zilizoendelea zinavyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake Nchi kwa mfano Korea Kusini, Mauritius lakini pia nchi kama Seychelles, wale wanafanya uvuvi wa ndani na kupitia uvuvi huo wanaingiza pato kubwa sana. Kwa hiyo mimi naamini kwamba tukianza sasa tukajenga hiyo bandari lakini pia tukanunua meli ya uvuvi tukaweza kuvua mpaka ndani ya bahari tutaweza kuinua uchumi wa nchi yetu kwa kasi kubwa sana. Kwa hiyo niombe sana jambo hili tulifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nakumbuka Mheshimiwa Zungu, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, amekuwa akilisemea sana hili jambo. Kwa hiyo niombe Serikali yangu muweze kufanyia kazi hili mapema ili angalau tuingie kwenye uvuvi ambao unaweza ukawa una manufaa kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme juu ya soko, hasa soko la zao la chai; kwa kweli sielewi kwa nini hatuleti ule mnada ambao unafanyika kule Kenya. Miaka mingi tumesema na wenzetu Wakenya wanafaidika sana kufanyia mnada kule kwa hiyo sisi tunazalisha chai nyingi na ni wazalishaji wazuri na tunazalisha chai bora, kwa nini tunapeleka kuuza Kenya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, inavyoonekana duniani inaonekana katika East Africa inayoongoza kuzalisha chai ni Kenya na chai ya Kenya ni bora, kumbe kwa sababu chai hiyo inauzwa Kenya. Kwa hiyo, niombe Serikali yangu, na Waziri wa Fedha na Waziri wa Kilimo mpo hapa, mfanye utaratibu wa kuhakikisha kwamba mnada wa chai ufanyike hapa hapa nchini. Ukifanyika hapa nina uhakika tutapata bei nzuri kuliko ilivyo sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kilo inauzwa shilingi 314, ni hela ndogo sana, lakini ikiuzwa hapa, mnada ukawa hapahapa nchini naamini hata zile kodi nyingine, kodi pengine za soko zile, zitabakia hapa hapa nchini. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali yangu tujitahidi tuhakikishe kwamba soko au mnada wa chai unahamia Tanzania haraka iwezekanavyo ili faida zinazotokana na kuwepo na huo mnada tuweze sisi Watanzania kuzipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyokwenda kuuza Kenya wanaofaidika ni Wakenya na sasa hivi karibia viwanda vyote wanachukua Wakenya. Sasa lazima tujiulize kwa nini wanachukua Wakenya hivi viwanda? Inawezekana pengine agenda ni hiyo kwamba tuendelee kuuza hiyo chai ule mnada uendelee kufanyika kule Kenya. Kwa hiyo niombe sana Serikali yangu, mimi naamini ni Serikali sikivu mtayafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya niunge mkono hoja, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja za Kamati hizi mbili. Nianze kwa kusema kwamba Kamati zimeandaa taarifa nzuri sana. Napongeza Kamati zote mbili; Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama lakini pia Kamati ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuishukuru sana Serikali kwa hoja waliyoitoa asubuhi kwa maana ya kauli ya asubuhi juu ya mauaji yaliyokuwa yanaendelea kule Njombe. Kwa namna ya pekee nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Naibu Waziri kwa namna wanavyoshughulikia hili jambo kwa ujirani mwema kabisa na kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba mauaji Njombe yanatokomezwa au yanadhibitiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Naibu Waziri, yeye aliweza kushiriki pia katika misiba kule Njombe, hasa ya wale watoto watatu pamoja na kuongea na wananchi na kutoa maelekezo mbalimbali kwa Jeshi la Polisi na viongozi wengine ili kwa pamoja kuweza kutokomeza mauaji yaliyokuwa yanaendelea kule Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, naomba nichangie kidogo kwenye nishati ya madini, hasa juu ya umeme vijijini kwa maana ya umeme wa REA. Kwanza, napongeza kazi zinazofanywa na Wizara hii, wanafanya kazi kubwa na tunaona matokeo; vijiji vingi vinaendelea kupata umeme na maendeleo kupitia umeme yanapatikana na viwanda vingi vinafunguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo ambako hii miradi inaendelea kwa sasa, bado kasi yake siyo kubwa, ni ndogo hasa tukiangalia kwenye mikoa yetu, hasa kwenye Jimbo langu, kasi ya usambazaji wa umeme ni ndogo. Naomba Serikali ijitahidi kuwapa Wakandarasi fedha ili waweze kuhakikisha kwamba wanasambaza umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo tayari kusambaza umeme lakini ukiwauliza tatizo kubwa linakuwa ni fedha, wanashindwa kupata fedha kwa ajili ya kununua nguzo na vifaa mbalimbali kama nyaya na transformer. Pia kuna tatizo la uzalishaji wa hivi vifaa. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri, wajitahidi kuhakikisha kwamba wale wazalishaji wa vifaa na fedha zinakwenda kwa wakati ili maeneo yote ya vijijini yaweze kupata huu umeme wa REA. Ni muhimu sana na nina uhakika kabisa itatubadilisha Tanzania baada ya muda siyo mrefu Tanzania haitabaki kama ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kidogo juu ya Shirika la TANESCO. Shirika hili pia linakabiliwa na madeni mengi kama walivyoeleza Wajumbe na inavyoeleza taarifa, lakini ulipaji wake wa madeni hayo bado unakwenda kwa kasi ndogo. Naomba Serikali ilipe madeni kwenye shirika hili ili liweze kujiendesha. Ilivyo sasa hivi, inapotokea kuna tatizo ambalo linahitaji vifaa, wanunue transformer au vifaa kwa ajili ya kurejesha umeme kwenye eneo fulani, inachukua muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna maeneo mengine, kwa mfano, Nyanda za Juu Kusini, maeneo yetu yana mvua nyingi, kwa hiyo, umeme umekuwa ukiathiriwa, transformer nyingi zimekuwa zikiunguzwa na radi. Kwa hiyo, inapotokea transformer imeungua, inakuwa ni vigumu; na inachukua muda mrefu sana kurejesha umeme katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati, alikuja kwenye eneo langu akakuta tatizo kubwa sana la umeme kwenye maeneo ya muhimu; ya hospitali na maeneo ya vijiji kwenye Kata moja ya Ikuna, lakini alipofika alitoa kauli na akaleta ile transformer. Nashukuru sana kwa Wizara nzima, Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kuleta hii transformer. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lililopo sasa, mpaka leo hii ile transformer haijafungwa, sijaelewa wanakosa vifaa gani? Kwa hiyo, naomba mwezeshe hili Shirika la TANESCO ili liwe na uwezo wa kurejesha huduma haraka, kwa sababu linapochelewesha huduma, madhara yanakuwa makubwa. Viwanda vinasimama kufanya kazi na huduma haziwezi kuendelea kwa sababu umeme haupo. Likiwezeshwa vizuri litaweza kujitegemea na kuhakikisha kwamba umeme unarejeshwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo haya ya Nyanda za Juu Kusini kwa sababu kuna radi nyingi, napendekeza kama inawezekana, tutumie ule mfumo wa Shirika kama la CEFA ambalo wanajenga transformer zinajengewa ndani na sijawahi kusikia transformer ya CEFA imepigwa radi. Kwa hiyo, kwenye maeneo ya mvua tunaweza tuka-adapt ule utaratibu wa CEFA ili transformer…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa. Muda wako umekwisha.

MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa uongozi wake wa kutukuka kwa Watanzania. Nawapongeza pia Mawaziri, Mheshimiwa Suleiman Saidi Jafo na Kapteni Mstaafu Mheshimiwa George H. Mkuchika na Manaibu Waziri wote Mheshimiwa Josephat Kandege, Mheshimiwa Mwita Waitara na Mheshimiwa Dr Mary Mwanjelwa kwa kazi kubwa wanazozifanya usiku na mchana kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha miundombinu ya Shule za Msingi na Sekondari. Shule nyingi za msingi zimepatwa na ongezeko kubwa la wanafunzi, udahili wa wanafunzi wa darasa la kwanza umeongezeka. Ongezeko hili limesababisha upungufu mkubwa wa madarasa, hivyo, Serikali iongeze fedha za ujenzi wa madarasa. Wananchi hasa wa maeneo ya vijijini hawana uwezo wa kumudu kujenga madarasa mfano katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, shule nyingi hasa zilizojengwa zamani hazina madarasa ya kutosha, naiomba Serikali itusaidie au ituongezee fedha za ujenzi wa madarasa hata kwenye shule zilizojenga nyuma ya miaka ya 1970. Mfano wa shule kongwe ni Sovi (1950s), Lupembe (1950s) na Kanikelele (1970). Majengo ya shule hizo za msingi yamechoka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa sekondari ni muhimu sana shule zetu za sekondari za kati, kujengwa mabweni kwa ushirikiano wa Serikali na wananchi. Shule nyingine za kata hazina mabweni na majengo mengineyo muhimu kama vile majengo ya utawala na mabwalo ya chakula. Uwepo wa majengo hayo huongeza ufaulu wa wanafunzi. Wanafunzi wanakuwa huru kusoma wanapoishi bwenini na ufaulu wao huongezeka. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe shule ambazo hazina mabweni ni Shule za Sekondari ya Ninga, Ikuna na Mlunga, Kidegembye (bweni la wavulana), Lupembe (mabweni yaliyojengwa zamani (yamechakaa), Sovi (bweni la wavulana) na Itipingi (hakuna mabweni ya A-level).

Mheshimiwa Naibu Spika, Ukusanyaji wa Mapato; Halmashauri nyingi hazikusanyi mapato au zinakusanya chini ya makadirio, Halmashauri nyingi zinakusanya chini ya asilimia hamsini hii inatokana na:-

Moja inawezekana kuna uzembe wa ukusanyaji mapato na kupelekea kukusanya chini ya kiwango; au Pili, inawezekana wataalam waliopo katika Halimashauri zetu wanashindwa kubuni miradi ambayo itawaingizia kipato cha uhakika sambamba na hali ya Halmashauri zao au kutegemea vyanzo hivyo bila kutabiri uendelevu na vyanzo hivyo. Mfano wa Halmashauri za Mikoa ya Katavi, Kigoma, Mtwara na Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TASAF; naipongeza Serikali kwa kuendelea kuzisaidia kaya zenye kipato kidogo kupata mahitaji ya msingi na kuwawezesha kujikwamua kwenye wimbi la umaskini kupitia mpango wa TASAF. Kuna baadhi ya vijiji havikuingizwa kwenye mpango wa TASAF, tunaomba vijiji hivyo viingizwe kwenye mpango huu ili kuondoa malalamiko. Mfano, katika Halimashauri ya Wilaya ya Njombe kuna Kijiji cha Sovi kilirukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), wanafanya kazi kubwa sana. Watanzania zaidi ya asilimia 75 ni wakulima, kwa hivyo barabara za vijijini ndiyo tegemeo kubwa sana kwa wakulima hawa. Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ina jumla ya barabara za vijijini zenye urefu wa kilomita 582. Eneo la Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ni eneo la uzalishaji wa mazao mbalimbali kama vile chai, kahawa, miti ya mbao na nguzo, mahindi, maharage, nanasi, parachichi na mihogo. Mazao mengi kati ya hayo huzalishwa wakati wa mvua nyingi na ni kipindi hicho barabara hizo huharibika sana na kukwamisha shughuli za uzalishaji na usafirishaji wa mazao hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili barabara hizi ziweze kufikika na mazao kufikia kufika sokoni, ni muhimu kutenga fedha za dharura ili kufanya matengenezo ya muda kwenye barabara hizi hasa kwenye maeneo yenye mvua nyingi kama Jimbo la Lupembe. Mwaka huu kutokana na mvua kubwa iliyoanza kunyesha Mwezi Februari, mpaka sasa barabara nyingi hazipitiki. Kuna baadhi ya maendeo hata madaraja yamekatika mfano barabara ya Lole – Maduma na Kidegembye – Image. Madaraja ya barabara hizi yanatakiwa kujengwa upya, hivyo ni muhimu Serikali kuwaongezea bajeti Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) ili kusaidia kuchochea uchumi wa halmashauri na mkoa kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja za Wizara zote mbili.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupewa nafasi nami kuweza kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri wote, na Watendaji wote wa Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa namna wanavyofanya shughuli zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda, niongelee tu suala la barabara, suala la barabara, hasa barabara inayotoka Kibena, Lupembe, Madeke na hatimaye Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni barabara muhimu sana, ni barabara muhimu kwa sababu kwanza inaunganisha Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Morogoro kwa hiyo, Mkoa wa Njombe na Morogoro ulikuwa haujaungana muda mrefu sana, lakini kupitia barabara hii sasa utaweza kuunganishwa na hatimaye wananchi wa Njombe wataweza kusafiri kirahisi kwenda Morogoro na kusafirisha mazao yao na mambo mengine. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mchane tu.

MHE. JORAM I HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni muhimu sana kwa sababu mazao mengi yanayozalishwa Mkoa wa Njombe yanatokea Lupembe. Mazao kama, mbao, miti, chai, kahawa, matunda parachichi, matunda kama nanasi yanazalishwa sana kwenye barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama vile haitoshi, barabara hii pia kuna mazao mengine, kama mazao ya mahindi na maharagwe yanatoka kwenye eneo hili. Kwa hiyo, unaweza ukaona namna gani jinsi ilivyo ya muhimu sana, kwa uchumi wa Mkoa wa Njombe lakini pia uchumi wa Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, lakini pia Halmashauri ya Wilaya ya Njombe asilimia 80 ya uchumi wake unategemea sana hii barabara ya Lupembe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama vile haitoshi, barabara hii ya Lupembe inategemewa sana, kwa maana ya wakati wa kifuku. Hii barabara huwa haipitiki, kwa hiyo mazao kama nanasi ambayo yanalimwa eneo la Madeke, ukienda Madeke utakuta kuna mashamba mengi, kuna kama zaidi ya ekari, kuna kama estates hizi zipo kule lakini wakati kama huo ambapo mvua inanyesha mazao yale kule yanaozea shambani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili kuweza kuboresha uchumi na kuinua uchumi wa Mkoa wa Njombe lakini kuuinua uchumi wa Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ni muhimu sana hii barabara iweze kutengenezwa, lakini nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri na Manaibu Waziri lakini pia na Mheshimiwa Rais kwa kuiweka sasa kwenye mpango sasa tayari kutafutiwa fedha ianze kujengwa kwa kiwango cha lami, kwa hiyo, nawashukuru sana kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya mkishirikiana na watendaji wote wa wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo, barabara hii ikitengenezwa kwa kiwango cha lami, uchumi wa Njombe utakua, lakini pia uchumi wa nchi utakua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine niongee nalo kidogo juu ya minara ya simu kuhusu mawasiliano. Tuna changamoto pia ya minara ya simu katika eneo letu hasa maeneo ya Kata Mfiriga eneo la madeke, halifikiki mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo la Mfiriga, eneo la Idamba, kuna eneo la Ninga pia halifikiki mawasiliano. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, pamoja na jitihada nimeziona za Serikali mmetuletea mnara kwenye Kata ya Ikondo, tayari Ikondo imefunguka japo bado kidogo kuna matatizo kidogo ya kurekebisha, nafikiri mtayarekebisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tukipata minara hii pia, itasaidia sana kuboresha uchumi. Kwa sababu, uchumi lazima yawepo mawasiliano, mawasiliano ya barabara lakini pia mawasiliano ya simu, ili wananchi au wakulima kwanza waweze kusafirisha bidhaa hizo ambazo wanazalisha ziweze kufikia soko kwa wakati. Lakini pili waweze kuwasiliana na ambako masoko yanapatikana kwa hiyo tukiboresha barabara ikajengwa kwa kiwango cha lami, kwanza tutapunguza muda wa kusafirisha haya mazao kufikia soko, lakini pili wananchi wataweza kupata faida kubwa kwa sababu gharama za usafirishaji zitapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana, niombe kwa Mwenyezi Mungu lakini pia niombe kwa maana ya Mheshimiwa Rais na Waziri, nakuamini sana Mheshimiwa Eng. Kamwelwe na Manaibu wako Waziri na Watendaji wote mtahakikisha kwamba fedha zinapatikana ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami na hatimaye uchumi wa maeneo hayo uweze kupanda na mazao yaweze kufikia soko kwa wakati, lakini pia na ikiwekwa minara ya simu itatusaidia sisi Wakulima wa Lupembe kuweza kuwasiliana na soko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake, sasa hivi mambo ya ki-digitali, mambo ya teknolojia, lazima kuwe na mawasiliano na hatimaye uweze kuuza kwa wakati na uweze kufikia kujua soko liko wapi na uweze kuuza mazao yako. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana najua una kazi nyingi na unafanya mengi, lakini naomba utusaidie kwa haya mambo mawili makubwa ya barabara na hili la minara ili wananchi wetu wa Lupembe waweze kuuza mazao yao lakini waweze kusafirisha mazao yao na nguzo ziweze kufikia soko na hatimaye.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu hizi nguzo zinatumika kwenye usambazaji wa umeme, ili tusiwe na tatizo la nguzo, sisi tunalima miti mingi sana, na tunazalisha nguzo nyingi lakini pia zinauzwa kwa bei nzuri. Kwa hiyo, kumbe mkitengeneza hii barabara tutaweza kuuza nguzo na hatimaye tatizo la nguzo nchini litapungua kwa sababu zile nguzo zipo kule na zinapatikana na zinasafirishwa kirahisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema maneno hayo machache nishukuru sana kwa nafasi lakini niunge mkono hoja iliyopo mbele yetu, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uamuzi wake wa dhati wa kutekeleza Sera ya Tanzania ya Viwanda. Mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015 viwanda nchini vimeendelea kuongezeka kwa kasi kubwa na vya zamani vimeendelea kufufuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara na Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanazozifanya usiku na mchana. Mwenyezi Mungu aendelee kuwajalia afya njema katika kusimamia utekelezaji wa Sera ya Tanzania ya Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya Waziri na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara ni kutengeneza mazingira ya watu wanaotaka kuwekeza kwenye viwanda na biashara nchini. Kazi hiyo inaendelea vizuri na kwa weledi mkubwa. Wawekezaji wengi wa nje na ndani ya nchi wanapenda sana kuwekeza nchini lakini kuna shida ya usumbufu wa kupata vibali mbalimbali vya kuanzisha viwanda na biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Wizara ione umuhimu wa kuunganisha baadhi ya vibali au kodi. Pia vibali au kodi hizo zilipwe kupitia ofisi moja. Mfano wa kodi au vibali hivyo ni kama vile TFDA, NEMC, OSHA na kadhalika. Mwekezaji anapoenda kutafuta vibali hivi avipate kwenye ofisi moja. Tuwe na jengo moja la uwekezaji na biashara. Hali iliyopo sasa imewakatisha tamaa wawekezaji na wafanyabiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Ubinafsishaji nchini ilitekelezwa kwa shinikizo la Mataifa ya kibepari. Hivyo Tanzania ilitekeleza sera hiyo bila kuwa na uzoefu wa kutosha. Zoezi zima la ubinafsishaji halikufanyika kwa umakini na usahihi uliohitajika. Matokeo yake kuna mali za Vyama vya Ushirika ziliuzwa kwa wafanyabiashara bila hata kushirikisha Wanaushirika. Pia kuna maeneo viongozi wachache waliuza mali hizo bila ya vielelezo. Mfano fedha zilizopatikana hazijulikani zilirejea kwenye akaunti ipi?

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri ni Kiwanda cha Chai cha Lupembe. Kiwanda hiki kilikuwa ni kiwanda chenye umiliki wa asilimia 100 ya wakulima wa chai kupitia ushirika wao wa MVYUULU. Baadaye miaka ya 1970 Serikali ilipewa kuendesha kiwanda hiki lakini baadaye Serikali ambayo ilipewa jukumu la kukiendesha tu, ikamwuzia mwekezaji bila kufuata taratibu na kusababisha mgogoro ambao una miaka 12. Ushauri wangu ni kwamba ni vizuri Serikali ikatatue migogoro kama hii mapema ili viwanda hivi viendelee kuzalisha kwa tija kuliko ilivyo sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa Liganga na Mchuchuma ni muhimu sana kwa maendeleo ya viwanda nchini. Mradi wa Liganga ukikamilika tutatatua tatizo la kuagiza chuma nje ya nchi. Tutapata fedha za kigeni na chuma tutapata kwa bei rahisi. Nchi ya Ujerumani ilifanya mapinduzi makubwa ya viwanda miaka ya 1870 baada ya kuanza kuzalisha chuma na makaa ya mawe. Pia uwepo wa makaa ya mawe Mchuchuma utasaidia kupata nishati ya kutosha na ya bei nafuu. Hivyo mradi huu ni wa muhimu kwa maendeleo ya viwanda nchini. Ni vizuri Serikali ikaona umuhimu wa kuutengea fedha za kutosha na uweze kuanza mapema.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa Bagamoyo SEZ kama ilivyoelezwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira ni wa muhimu katika kufungua fursa za kiuchumi. Pamoja na umuhimu wake, ni muhimu sana kupitia mikataba tutakayoifunga na mwekezaji isije ikatokea kama ilivyo kwenye nchi za Zambia, Sri Lanka, Eritrea na Namibia. Hivi sasa nchi hizo zimejikuta ardhi yao inamilikiwa na China. Mikataba mibovu itatuingiza kwenye Ukoloni Mamboleo. Naishauri Serikali tuendelee kupitia kwa umakini mikataba tunayotarajia kuifunga na wawekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vidogo vidogo (SIDO). Viwanda hivi ni vya muhimu sana kwa maendeleo ya viwanda na ukuaji wa uchumi wa nchi. Viwanda hivi ndivyo vinavyoajiri watu wengi nchini. Serikali ione umuhimu wa kuongeza bajeti. Nchi zote zilizoendelea duniani zilianza na kuimarisha viwanda vidogo vidogo. Naishauri Serikali iweke utaratibu wa kutoa mikopo kwa watu au vikundi vyenye nia ya kuanzisha viwanda vidogo vidogo ili mazao yanayozalishwa yaweze kuongeza thamani kupitia viwanda hivi vya SIDO.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua fursa hii kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wake kwa kazi kubwa ambazo wanazifanya usiku na mchana, kwa kweli wanafanya kazi. Naomba Mwenyezi Mungu aendelee kuwalinda ili muendelee kufanya kazi zaidi kuwaletea maendeleo Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sekta ya Nishati ndiyo sekta wezeshi kwa maana ya viwanda nchini na nchi yoyote ambayo imeendelea kiviwanda ni lazima iwe na umeme wa kutosha. Kwa hiyo, naamini kwamba mipango iliyopo ya Wizara na miradi hiyo ambayo inakwenda kuanzishwa itasababisha nchi yetu iwe na viwanda vya kutosha na hatimaye kuongeza uchumi wa wananchi lakini pia nchi yetu kukua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie juu ya usambazaji wa umeme, hasa kasi ya wakandarasi. Kasi ya wakandarasi wa umeme kwenye maeneo mengi siyo nzuri, hairidhishi. Kwa mfano kwenye jimbo langu mpaka sasa hivi kuna kata tatu hazina umeme kabisa lakini pia mkandarasi aliyepo kwenye eneo langu alianza kazi toka mwaka jana lakini mpaka leo hii ameweza kupeleka umeme kwenye vijiji viwili na katika vijiji hivyo viwili amepeleka kitongoji kimoja kimoja; amepeleka umeme Kijij cha Hang’ana kitongoji kimoja, lakini poa Kijiji cha Iyembela kitongoji kimoja, lakini bado kwenye maeneo mengi hajapeleka umeme. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri tusaidie ili kasi ya mkandarasi iweze kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya maeneo wananchi wameshajituma tayari kuanza, wameitikia agizo la Mheshimiwa Rais la Tanzania ya viwanda tu. Kwa mfano Kijiji cha Ndinga wana kiwanda cha sembe wamenunua toka mwaka 2016 lakini mpaka leo hakifanyi kazi kwa sababu wanasubiri umeme uweze kufika katika kijiji hicho.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tuna Kijiji cha Madeke, wana kiwanda cha kuchakata mananasi, bado hakifanyi kazi kwa sababu umeme haupo. Wamejaribu kutumia nishati ya dizeli, dizeli ni gharama; lakini pia wametumia solar, haina uwezo mkubwa wa kuweza kustahimili kwa sababu kule eneo la Lupembe ni eneo la mvua nyingi kwa hiyo muda mwingi ni mvua kwa hiyo haiwezi kustahimili kuweza kuzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tukuombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye maeneo haya ya uzalishaji kwenye maeneo ya vijiji hivi, kasi iweze kuongezeka ili wananchi wa Jimbo hili la Lupembe waweze kupata umeme na hatimaye kuweza kuanzisha viwanda kwa sababu ni wakulima wa matunda, ni wakulima wa mananasi, ni wakulima wa miti, kwa maana ya mbao, wanataka viwanda ili kuweza kuongeza thamani ya mazao yao.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni juu ya umeme ambao unapelekwa kwenye viwanda. Eneo letu la Lupembe ni eneo la mvua nyingi na tuna viwanda vikubwa, hasa viwanda vile vya chai, tunavyo viwanda viwili katika eneo lile. Lakini pia viwanda vingine watu wanataka kuwekeza wanashindwa kwa sababu maeneo mengi hakuna umeme.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tuna tatizo moja kwenye viwanda, kwamba umeme unapokuwa umekatika, kwa mfano transfoma inapokuwa imeungua, wamiliki wa viwanda wanatakiwa kununua hizo transfoma, kwa hiyo, imekuwa shida sana. Mara nyingi utakuta kwamba transfoma ikikatika zinaisha wiki moja mpaka mbili hawana transfoma na wananchi wanachuma chai hawawezi kuuza kwa sababu kiwanda hakifanyi kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuombe sana; utaratibu huu wa kwamba wawekezaji ndio wanunue transfoma naona kama siyo mzuri. Ni vizuri TANESCO wawe wananunua hizi transfoma ili zinapokatika basi waweze kurudisha haraka ili wakulima waweze kuendelea kuuza chai yao, waweze kuendelea kuuza mazao yao na waweze kupata faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ilivyo sasa hivi, kwa mfano zao la chai likichumwa tu lazima likauzwe na lazima lichakatwe siku hiyo hiyo, likilala siku ya pili chai inapoteza ubora na itakuwa ni ya kumwaga tu. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, hasa kwenye maeneo haya ya uzalishaji kwenye maeneo kama ya viwanda vya chai; TANESCO wawe na transfoma zao na ikiwezekana wawe na transfoma za akiba ili pale ambapo umeme unakuwa umekatika basi waweze kuzipeleka haraka ili wakulima ambao wamechuma zile chai zao waweze kuuza siku hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu mwekezaji yeye anaangalia faida tu, ukikatika umeme anakwambia umeme haupo kwa hiyo leo hatuchukui chai. Kwa hiyo, mwisho wa siku wanaopata hasara kubwa ni wale wakulima ambao wamechuma hiyo chai na mazao mengine. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, tuwe na utaratibu kwenye viwanda hivi tuwe na transfoma za akiba.

Mheshimiwa Spika, niseme juu ya umeme, hasa umeme unaozalishwa na makaa ya mawe pale Mchuchuma. Nikuombe sana Mheshimiwa, huu mradi ni wa muhimu sana kwa sababu umeme ule utakuja kutusaidia muda ambapo maeneo mengine au vyanzo vingine vitakuwa haviwezi kuzalisha umeme.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Dkt. Merdad Kalemani, Waziri wa Nishati na Mheshimiwa Subira Mgalu, Naibu Waziri wa Nishati kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kutumikia Watanzania kwa kuhakikisha kaya zote nchini zinapata umeme. Mungu awabariki sana. Pia nawapongeza Watendaji wote wa Wizara kuanzia Katibu Mkuu, Dkt. Khamis Mwinyimvua, Wakurugenzi na Mameneja wote wa Mikoa.

Mheshimiwa Spika, sekta ya umeme au nishati ni muhimu sana kwa maendeleo ya viwanda nchini. Ukuaji wa sekta ya viwanda unategemea sana uwepo wa nishati ya umeme wa kutosha na wa bei nafuu. Nchi kama Marekani, China, Japan na South Korea zimepiga hatua katika maendeleo ya viwanda ni kutokana na uwepo wa vyanzo vingi vya umeme.

Mheshimiwa Spika, kasi ya usambazaji wa umeme kwa baadhi ya maeneo ni nzuri lakini kuna maeneo kasi ya usambazaji ni ndogo sana. Mfano, katika Jimbo la Lupembe speed ya Mkandarasi wa REA ni ndogo sana. Tuna vijiji 22 havina umeme lakini tangu mwaka jana 2018, Mkandarasi ameanza kusambaza umeme katika vijiji viwili tu na kila kijiji amesambaza kwenye mtaa mmoja tu katika Vijiji vya Ihang’ana na Iyembele. Pia amepeleka nguzo katika Kijiji cha Ninga tangu mwezi Januari lakini mpaka sasa kazi haijaanza.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Lupembe kuna wakulima wengi wa mazao ya chai, matunda, miti ya mbao, mahindi na parachichi. Mazao haya yanahitaji viwanda vya kuongeza thamani lakini tatizo limekuwa umeme. Mfano, wakulima wamenunua kiwanda cha sembe katika Kijiji cha Ninga tangu 2016, lakini hakijaanza kufanya kazi kutokana na kukosekana kwa umeme. Pia wakulima wa nanasi wa Kijiji cha Madeke wana kiwanda cha kuchakata nanasi, lakini kiwanda hakifanyi kazi kutokana na kukosekana kwa umeme. Hivyo ni muhimu kuangalia uwezo wa hawa Wakandarasi kwani wanakwamisha juhudi zote za Waziri na Naibu Waziri za kuwaletea maendeleo wakulima kupitia huduma ya umeme.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto kwenye maeneo ya viwanda umeme unapokuwa umekatika kutokana na kuungua kwa transformer. Wawekezaji wamekuwa wakiambiwa wanunue transformer wenyewe na wajiunganishie, hii imekuwa ikiwaathiri wakulima. Mfano, Jimboni kwangu Lupembe tuna viwanda viwili vya chai na kutokana na eneo la Lupembe kuwa na mvua nyingi zinazoambatana na radi hupatwa na tatizo la kuungua kwa transformer na kiwanda kutoendelea kufanya kazi mpaka transformer ipatikane, wakati mwingine huchukua wiki mbili mpaka tatu.

Mheshimiwa Spika, hii imekuwa ikiathiri wakulima wa chai na kupoteza uchumi wa wakulima hawa, hivyo nashauri Wizara kwenye maeneo ya viwanda tuwe na transformer za ziada au za akiba ili pindi kunapotokea kuungua kwa transformer kufanyike replacement mapema ili kuokoa uchumi wa wakulima hawa. TANESCO wapeleke transformer na wafunge kuliko kuwaachia wawekezaji wajitafutie transformer zao wenyewe.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze Wizara kwa kutoa offer ya punguzo la bei ya kuunganishiwa umeme kwa bei ya shilingi 27,000 kwa REA na TANESCO, hili litaharakisha usambazaji wa umeme vijijini. Nashauri Mheshimiwa Waziri awaagize Mameneja wote wa TANESCO kwa kutoa waraka maalum na Wabunge wapate nakala yake. Hii ni kutokana na kwamba bado wananchi kwa baadhi ya maeneo wanakataliwa kulipia, wanaambiwa kulipia mpaka kuwepo na nguzo ya kuingizia umeme kwenye nyumba yake kumbe wangelipia hizi fedha zingesaidia kununua waya, nguzo na vifaa vingine, lakini pia wananchi wengi wakipata umeme wananchi watalipia bili za umeme na shirika litaongeza makusanyo ya fedha.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Umeme wa Makaa ya Mawe wa Mchuchuma; mradi huu ni muhimu sana kwa maendeleo ya viwanda nchini. Mradi wa Mchuchuma ukianza utatusaidia kupata umeme wa bei nafuu na wa kutosha, lakini kupitia mradi huu tutapunguza makatizo ya umeme yanayotokea wakati wa kiangazi au mvua inapopungua na shughuli za uzalishaji zitaendelea vizuri kwa kuwa kutakuwa na umeme wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, scope ya miradi ya umeme kwa baadhi ya maeneo ni ndogo sana. Wakandarasi wamekuwa wakieleza kwamba usambazaji wa umeme unategemea scope waliyopewa. Kuna vijiji ni vikubwa sana mfano, katika Jimbo la Lupembe, scope ikiwa ni kilometa mbili maana yake itatosha kitongoji kimoja tu na hivyo eneo au kitongoji kilichokosa umeme kuanza kulalamika kwa kutopata umeme hivyo ni muhimu kuangalia na aina ya kijiji chenyewe ili angalau kuwapa umeme wananchi wote waliopo kwenye kijiji hicho. Hii itasaidia kuondoa lawama na manung’uniko kwa sisi viongozi wa kuchaguliwa.

Mheshimiwa Spika, mwisho, narudia kuwapongeza sana Waziri na Naibu Waziri kwa kujituma kwao katika kuhakikisha kila kaya inapata umeme. Wanafanya kazi kwa kujituma kama vile ni kazi zao binafsi, kwa kweli wamekuwa mfano mzuri wa kuigwa na Wizara nyingine. Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia kidogo juu ya Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Taarifa wa mwaka 2016 (The Access to Information Act, 2016).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Katiba na Sheria na Serikali kwa ujumla kwa kuuleta huu Muswada wakati huu. Muswada huu umekuja kwa wakati muafaka kabisa ambapo Watanzania wengi wanahitaji kupata taarifa. Pia Muswada huu unaendana kabisa na kauli mbiu ya Serikali ya „Hapa Kazi Tu‟ kwa maana ya dhana ya uwajibikaji na uwazi. Kwa hiyo, kwa kuwa na Muswada huu kutasaidia kuhakikisha kwamba kunakuwa na uwazi kwenye Serikali zetu hasa kwenye Halmashauri zetu ambako huko ndiko kuna matatizo mengi hasa ya utoaji wa taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwamba inasaidia Viongozi wetu kwa maana ya Watendaji wetu wa Halmashauri na Taasisi mbalimbali za Serikali kuweza kutoa taarifa mbalimbali zinazohusu mikakati ya maendeleo, mapato na matumizi, mipango yao na miradi yao ya kimaendeleo katika maeneo yao. Hizi ni taarifa muhimu sana kwa wananchi kuzipata ili waweze kujua nini Serikali imepanga na Halmashauri zao zimejipanga namna gani kwa ajili ya maendeleo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa kupata taarifa hizi zinawasaidia wananchi au Serikali kuhakikisha kwamba kero mbalimbali za wananchi zinapunguzwa. Hivyo sasa hivi ukipita katka maeneo mengi hasa vijijini, utakuta wananchi wanalalamika hawapewi taarifa ya miradi, hawapewi taarifa za mapato na matumizi kwenye vijiji vyao. Kwa hiyo kwa kuweka sheria hii kwa kupitia Muswada huu utawawezesha hawa viongozi wetu walioko huko chini waweze kutoa taarifa mapema na hivyo wananchi kuwa na uelewa wa mambo ambayo yanaendelea kwenye maeneo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali kwamba ni muhimu sasa Serikali itengeneze utaratibu mzuri kuwe na client service charter kwa kila taasisi ili kupitia hizo wananchi au watafuta taarifa au walaji wa taarifa wajue watazipataje hizo taarifa na hizo taarifa zinapatikana kwa muda gani. Kama tulivyoona wengi huwa wanalalamika kwamba taarifa zinachelewa, mtu anakwenda ofisini anaambiwa uje kesho, uje keshokutwa au uje mwezi ujao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kukiwa kuna clients service charter hii na wananchi wakijua, kwa sababu ile inaonesha ni taarifa ipi itapatikana kwa muda gani. Kuna taarifa nyingine za saa moja au siku moja, kuna nyingine za wiki moja, wiki mbili na nyingine za wiki tatu, wakishajua utaratibu huu ukiwepo kwenye Taasisi zote za Serikali inakuwa rahisi kujua yule mtu anayetafuta taarifa kujua hii taarifa nitaipata kwa muda gani, kuliko ilivyo sasa hivi. Kwa hiyo, niombe Serikali iweke utaratibu kuhakikisha kwamba kila Ofisi ya Serikali, kila ofisi zinazohusika na Sheria hii au na Muswada ambapo itakuwa Sheria basi iwe na clients service charter kwa ajili ya kuwawezesha watu kujua ni lini watapata taarifa zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja juu ya utunzaji wa taarifa. Imetajwa kwamba angalau taarifa zikae kwa muda wa miaka 30. Kwangu naona ni muhimu kwamba tuwe na utunzaji wa taarifa kwa kuwa taarifa zikitunzwa vizuri zinatusaidia baadaye. Watu wengine wanatumia hizi taarifa, ripoti mbalimbali na taarifa mbalimbali kwa ajili ya kufanya tafiti mbalimbali, pia taarifa hizi zinatumika pengine kwa ajili ya kupata historia ya jambo fulani lililotokea mwaka fulani au maamuzi yaliyowahi kufanyika muda fulani na watu fulani au taasisi fulani au Serikali. Hivyo, ni muhimu kuwa na utunzaji wa taarifa wa muda mrefu ili zitumike kwenye mambo ya historia, lakini pia ziweze kutumika kwa ajili ya tafiti mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nilisemee kidogo ni juu ya hizi taarifa. Tumesema kwamba zitatumika kwa Serikali au kwa Taasisi za Serikali zinazonufaika na Serikali au zilizo chini ya Serikali, haijasema kwamba je, taasisi nyingine ambazo siyo za Serikali ambazo ni taasisi za binafsi au tunaita taasisi zisizo za Serikali kama vile makampuni mbalimbali. Kuna makampuni mengi hapa nchini ya uwekezaji kwa aina mbalimbali, Muswada hauelezi vizuri jinsi gani hawa walaji wa taarifa wataweza kupata taarifa kwenye Taasisi hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiiacha ikaelea elea hivi itakuwa shida sana kupata taarifa kwenye makampuni kwa sababu wanasema hii sio taasisi inayosimamiwa na Serikali, ni taasisi binafsi, ambayo inajitegemea. Kwa hiyo ni muhimu hii Sheria ifafanue vizuri. Tutamwomba Waziri atakapokuja kufanya majumuisho basi afafanue vizuri ni sehemu gani zina-cut across hii Sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri ni muhimu sana kwenye taasisi hizi zisizo za Serikali nazo pia ziweze kutoa taarifa, kwa sababu wananchi wanahitaji kujua haya mashirika pengine yasiyo ya Kiserikali yanafanya nini na baadhi ya taarifa ni muhimu sana kwao. Kwa hiyo, ni muhimu kukawa na utaratibu au Sheria ikawagusa ili nao waweze kutoa taarifa na wananchi waweze kunufaika na hizi taarifa ambazo watakuwa wanazitafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna jambo la adhabu, imeelezwa hapa kwamba adhabu kwa atakayekuwa ametoa taarifa zile zinazohusu mambo ya usalama, basi kifungo itakuwa ni miaka 15 na isiyozidi miaka 20. Naunga mkono hiyo, pia kwa wale ambao watakuwa wametoa taarifa nyingine kwa mfano wamepotosha taarifa na tunajua sasa hivi ilivyo, magazeti mengi yanapotosha taarifa, vyombo vya habari vingi vinapotosha taarifa, ni muhimu kumbe wawe na hii adhabu kwamba angalau basi anayekuwa amepotosha taarifa ataenda kifungo cha miaka mitatu na kisichozidi miaka mitano. Kwa hiyo, naomba hii pia tuiwekee utaratibu mzuri na makosa yaainishwe vizuri ili mtu anapohukumiwa asilalamike kwamba adhabu pengine imezidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Muswada ni mzuri na umekuja kwa muda muafaka na unaofaa sasa hivi kwa jinsi hali ilivyo na mahitaji ya jamii yetu yalivyo. Kwa hiyo, naunga mkono hoja, naunga mkono Muswada huu uweze kupitishwa vizuri na uanze kufanya kazi haraka sana. Ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali, 2017
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Muswada huu. Kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri wa Fedha kwa kuleta Muswada huu sasa baada ya kuona kama alivyosema msemaji wetu wa kwanza, Mheshimiwa Mhagama, baada ya kufanya tathmini kuona kwamba practically utaratibu wa zamani hauleti tija, basi ameamua kuja na marekebisho haya ili tuweze kuisaidia Serikali na Wizara iweze kuwa na tija katika kutoa taarifa zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashangae baadhi ya Wajumbe wa Kamati hasa upande ule wanaolalamika juu ya Muswada huu. Tumefanya kazi wote na Waziri amekuja na maelezo mazuri na Mwanasheria Mkuu ametoa ufafanuzi mzuri, Kamati tukaelewa, tukaona umuhimu wa kukubaliana na marekebisho au kukubaliana na haya maombi ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshangaa dada yetu pale, mama yetu Riziki. Ndiyo matatizo ya kuwa mtoro kwenye Kamati, ungekuwepo jana ungepata taarifa vizuri. Kwa hiyo, nikubaliane na Muswada huu, ni utaratibu wa kawaida popote pale kwa Serikali zote duniani, marekebisho ya baadhi ya Sheria kama tunavyosema kwamba ni progressive process kwa hiyo kilichofanyika…

T A A R I F A...

taarifa kwa sababu kikao cha jana kilikuwa ni muhimu sana kwetu Wanakamati na ndiyo maana tumekuja na msimamo huu kama Kamati kwa sababu yale yaliyoletwa jana na Waziri na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ndiyo iliyotujengea tuweze kuamini kwamba huu Muswada ni wa muhimu kuupitisha, kwa hiyo ndugu yangu hukuwepo basi ndiyo maana mambo yamekupita. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshaona hata kwenye halmashauri zetu taarifa zetu, kama huwa mnahudhuria vikao
Waheshimiwa Wabunge mnaweza mkajifunza tu kwenye halmashauri, kwenye halmashauri Kamati za Fedha na Mipango zinakaa kila baada ya miezi mitatu mitatu, unaweza ukajifunza jinsi gani taarifa zile zilivyo, unakuta zina matatizo mengi. Sasa je, katika National Level kwa maana ya Wizara na Wizara hizi zinategemea kupata taarifa hizi kwenye taasisi mbalimbali za Serikali, mojawapo ikiwa ni halmashauri, kunakuwa na matatizo makubwa. Kwa hiyo, ni kweli kabisa Serikali isingeweza kufanya majukumu yake vizuri na wasingeweza kuja kuwa na taarifa nzuri kama sehemu ambazo wanategemea kupata taarifa hizi kama taarifa za mapato na matumizi, zinakuwa siyo realistic.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nipongeze Wizara kwa kuja na utaratibu huu wa miezi sita, kuna uhakika kwamba Serikali itakuwa na muda wa kutosha wa kufanya kazi. Itafanya kazi angalau miezi mitano na ule mwezi mmoja wata-complied taarifa na sisi Wabunge tutapata taarifa ambazo zimekuwa realistic, taarifa ambazo ni za uhalisia. Kwa hiyo, hiyo ni moja ya faida ambayo tutaipata kupitia Muswada huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, huu ni utaratibu wa makampuni mengi makubwa, makampuni ya kimataifa, lakini ni utaratibu hata wa nchi nyingine, Wabunge wengi mmezunguka nchi mbalimbali, kama mmewahi kukutana na Mawaziri au kujifunza taratibu za uwasilishaji wa bajeti, utakuta mara nyingi wanawasilisha mara mbili kwa mwaka. Kwa hiyo na sisi tunajifunza which are the best practices toka kwenye nchi nyingine. Kwa hiyo hii itasaidia pia kuhakikisha kwamba Serikali yetu inaweza ikatoa taarifa vizuri, taarifa ambazo hazina walakini, taarifa ambazo hazina upungufu, kwa hiyo nami pia naunga mkono hoja hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ni gharama, Waziri amekuwa akichapisha vitabu hapa vinajaa pale kwenye Pigeonholes zetu, hatusomi wakati mwingine, lakini tukiwa na taarifa mbili, vitabu viwili tunakuwa na muda wa kusoma vizuri. Vile vile tunapunguza gharama kwa Serikali ya kuchapicha vitabu. Pia tutapunguza gharama ya muda ambao watumishi wetu wa Serikali wanakaa kwa ajili ya kuandaa taarifa, kila baada ya miezi mitatu wanaandaa taarifa. Ni gharama ya muda, lakini pia financial cost, kuna financial cost implication pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme kwamba naunga mkono hoja kwa utaratibu huu ili tuweze ku-save gharama ya muda lakini pia tuweze ku-save gharama za kuchapisha vitabu. Vilevile niunge pia mkono kwa hii sheria kutaja ni nini kitafanyika kwa afisa yeyote ambaye hatatekeleza majukumu yake vizuri maana yake hapa ungeweza kutokea uzembe. Kwa hiyo, niunge mkono kwamba Sheria imesema vizuri kwamba huyu Afisa atakatwa mshahara wake wa miezi sita, lakini pia na taratibu nyingine za kijinai zitachukuliwa. Hii itawafanya pia watumishi wetu ambao wana jukumu la kuandaa taarifa waweze kuwa makini katika uandaaji wa taarifa na wahakikishe kwamba wana-meet deadline iliyotolewa na Wizara kuwasilisha taarifa hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Naomba Sheria iweze kupitishwa vizuri ili ianze kufanya kazi.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 5) wa Mwaka 2017
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia Muswada uliopo mbele yetu. Nami nianze kuipongeza Serikali kwa kuleta mabadiliko haya, ni ya muhimu sana kwa kufikia malengo ya Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite pale kwenye Sheria ile ya Ardhi ya Marekebisho, Sura ya 113 (The Land Act CAP, 113), masharti yanayohusu matumizi ya ardhi, hasa kwenye kupata mikopo kwa maana ya mortgage. Ni kweli tumeona wawekezaji wengi wamekuwa wakitumia ardhi kwa ajili ya kupata fedha kupata mikopo kwenye benki mbalimbali za ndani na nje ya nchi. Hata hivyo, fedha hizi mara nyingi zimekuwa haziendi kwa ajili ya kuendeleza maeneo au mashamba yale ambayo wamekopea fedha na badala yake wamekuwa wakifanyia shughuli nyingine au wamekuwa wakipeleka nje kuwekeza huko nje ya nchi na hatimaye sisi kama nchi tumekuwa tukikosa ajira kwa maana ya yale mashamba ambayo wamekopea fedha yamekuwa hawaendelezwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa mfano mengi ya mashamba ya mikonge yaliyopo kule Tanga, mashamba ya chai yaliyopo Tanga na maeneo ya Lupembe kule; unakuta watu wamekopa fedha nyingi, lakini fedha hizi hazitumiki kuendeleza mashamba haya na hatimaye tunakosa ajira kwa vijana wetu, lakini pia tunakosa fedha ambazo zingetokana na kuuzwa yale mazao na kupata fedha za kigeni. Kwa hiyo, kimsingi uchumi wa nchi unaharibiwa na hawa wakopaji ambao wanakopa lakini wanaenda kufanyia mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sheria hii ni nzuri, itasaidia kuhakikisha kwamba fedha zinazokopwa, hasa kwa
mashamba yale ambayo hayajaendelezwa ili yaweze kuendelezwa na yale ambayo yameendelezwa kidogo basi yaweze kupanuliwa zaidi. Kwa hiyo nimeona hii sheria ni nzuri na itasaidia kuhakikisha kwamba fedha zinawekezwa nchini na hatimaye uchumi wa nchi unakuwa tofauti na ilivyokuwa hapo mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nichangie na Sheria hii ya Utumishi wa Umma ambayo inahusu kuongeza muda wa kustaafu, kwa maana ya maprofesa, wahadhiri waandamizi, lakini pia na madaktari bingwa. Ni kweli, wanasema wataalam kwa uzoefu kwamba daktari bingwa au mhadhiri mwandamizi au profesa jinsi umri unavyozidi kusogea basi uzoefu unaongezeka. Kwa hiyo kwa kufanya hivi itatusaidia maprofesa, wahadhiri waandamizi na madaktari bingwa kuweza kuwawezesha wale wengine ambao hawana uzoefu wa kutosha waweze kuwapa uzoefu wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona pia sheria hii imefuata nchi nyingine jinsi wanavyofanya, kwa mfano Nchi ya Kenya, wao madaktari bingwa hasa waliopo kwenye hii fani ya tiba wanastaafu kwa hiari katika umri wa miaka 70 na kwa lazima miaka 75. Pia ukiangalia Nchi ya Nigeria, madaktari na maprofesa wanastaafu kwenye umri wa miaka 70; Botswana nao wanastaafu kwenye umri wa miaka 65 na nchi nyingine kama Zimbabwe wanastaafu miaka 65.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa na sisi pia tutakuwa sawasawa na nchi nyingine kwa maana ya hawa maprofesa, wahadhiri waandamizi na madaktari bingwa, kwa hiyo tutaendana sambamba na nchi nyingine. Maana yake wataalam wetu wengi wamekuwa wakistaafu katika umri wa miaka 55 wanaondoka kwenda kusaidia nchi nyingine ambako wanaendelea kustaafu mpaka miaka 70.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona madaktari bingwa nao wamekuwa wakiamua kustaafu mapema ili waweze kuingia kwenye mkataba na hatimaye waweze kulipwa pensheni lakini pia wanaanza kulipwa ule mkataba, kwa hiyo
imekuwa ni gharama kubwa sana kwa Serikali. Kwa hiyo kwa kuongeza muda maana yake tunatatua tatizo la kulipa gharama kubwa kwa ajili ya mikataba ambayo tungewapa hawa madaktari ambao wamefikia miaka 55 au wamefikia miaka 60, wameshastaafu tayari; kwa hiyo kwa mtindo huu tunaokoa gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sasa Serikali katika mipango yake ni vizuri ijipange vizuri kuhakikisha kwamba inaweka mpango wa muda mrefu wa kuhakikisha kwamba wanaanza kuwaandaa hawa madaktari bingwa mapema au wanaanza kuwaandaa hawa wahadhiri waandamizi mapema ili kusijitokeze tena haya matatizo ambayo yamejitokeza katikati kuwa na… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalam ya Walimu Tanzania wa Mwaka 2018
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, pia kuwaombea wanafunzi wote wa darasa la saba ambao wameanza kufanya mitihani yao leo. Mwenyezi Mungu awajalie afya njema ili waweze kumaliza mitihani vizuri na hatimaye waweze kufaulu vizuri na kwenda sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara ya Elimu kwa kuleta Muswada huu muhimu sana kwa walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge ambao ni walimu tuliopo humu ndani tumekuwa tukiulilia kwa muda mrefu tangu tulipoanza Bunge hili kwamba tunaomba tuwe na Bodi ambayo itasimamia masuala ya walimu (Teacher’s Professional Board). Hatimaye leo tunafurahi kwamba Mheshimiwa Waziri ameileta na naipongeza Kamati kwa kuijadili na kuja na mapendekezo mazuri sana ambayo yapo kwenye Muswada huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Walimu ni muhimu sana na huu Mswada ni wa muhimu sana kwa walimu kwa sababu kumekuwa na makundi ya walimu. Kama wenzangu walivyosema, ni kwamba kuna walimu wale ambao wanafanya kazi kwenye shule zisizo za Serikali na wale ambao wanafanya kazi kwenye shule za Serikali. Wale wanaofanya kazi kwenye shule zisizo za Serikali walikuwa wanaonekana kama weak hivi au hawakutambulika kwa sababu wenzao wa Serikali wanapewa cheque number na wanatambulika, lakini hawa waliopo kwenye shule za watu binafsi, wamekuwa wakifanya lakini bila kutambulika na wakati mwingine wanashindwa kupata stahili kwenye baadhi ya maeneo. Kwa hiyo, sasa kupitia hii Bodi sasa walimu hawa watatambulika kama walivyo wenzao kupitia usajili. Kwa hiyo, napongeza sana hili na litatusaidia sana kuhakikisha kwamba walimu wetu wote kuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, wenzangu wameeleza vizuri kwamba uwepo wa Bodi hii ya Walimu itakayosimamia mambo taaluma za walimu, itatusaidia sana kuwaondoa wale walimu ambao hawana vyeti, wale walimu ambao wamekuwa wana matatizo sehemu nyingine, wakipata matatizo kwa mfano Serikalini, wamekuwa wakikimbilia kwenye shule za watu binafsi, kwa sababu kule hawawezi kurudi kwa sababu ya yale matatizo. Kwa hiyo, sasa kumbe kupitia huu usajili ambao utafanyika kila mwaka, wataweza kubainishwa na hatimaye kuondolewa kabisa kwenye utumishi wa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna moja ama nyingine imekuwa ni moja ya sababu inayochangia pengine utovu wa nidhamu, lakini pia kushuka kwa maadili katika shule zetu hizi za Tanzania. Kwa sababu watoto wanaofundishwa wote wanakuwa ni Watanzania na wanaingia kulelewa na mwisho wa siku wanamaliza chuo na wanakuja kufanya kazi kama watoto wengine. Kwa hiyo, ni muhimu sana hawa walimu kwanza tujue taaluma zao vizuri, wakaguliwe, waweze kusajiliwa na kupitia huo usajili waweze kufanya kazi vizuri na hatimaye kuwalea watoto wetu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna kitu kibaya sana kama kutomlea mwanafunzi vizuri hasa wale watoto wa chekechea. Sasa hivi kwenye vituo vyetu vya elimu hasa kwenye vituo vile vya Day Care na Nursery Center, kuna walimu wengi hawajapitia mafunzo ya ualimu wa awali lakini wanafundisha. Kuna wengine wameishia form four, kuna mwingine amefika form six anaanzisha kituo chake cha Day Care, mwisho wa siku huyu mtoto kwa sababu kile kituo kimesajiliwa, anapokelewa kwenye mfumo rasmi kwa maana ya shule za Serikali wakati amekosa maadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi ambacho mtoto tunamlea vizuri kujitambua lakini pia kuwa na maadili mema, tunaanza kumlea anapokuwa kwenye shule za awali pale chini ndipo malezi ya mtoto yanapoanzia, siyo huku juu. Kwa hiyo, ni lazima tuwe na watu ambao tuna uhakika kwamba hawa watu wana sifa stahiki za kuweza kuwasaidia watoto wetu waweze kupata maadili mema ya Kitanzania lakini pia waweze kufundishwa na kuandaliwa vizuri kwa ajili ya masomo ya shule ya msingi, baadaye sekondari na hatimaye vyuo vikuu. Kwa hiyo, ni muhimu sana na Bodi hii ndiyo mwarobaini wa tatizo hili la maadili kwa watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine pia ni kudhibiti maadili ya walimu. Tumesikia mara nyingi na Waheshimiwa wamesema hapa kwamba kuna baadhi ya walimu wanatoa adhabu zisizostahili, ni kwa sababu pengine hawajafundishwa, hawajaenda vyuoni. Kuna clip hapa nimeiona, mwalimu ameshika kiboko, anachapa wanafunzi
nafikiri sijui ni wa form four au form five, anawachapa viboko mgongoni na kichwani, sasa huyu sio mwalimu. Tunaojua ualimu huwezi kumchapa mtoto mgongoni wala kichwani, lakini kuna mwalimu anafanya hivyo. Kwa nini? Inawezekana huyu mwalimu sio mwalimu, hajapata maadili ya ualimu, hajapata kufundishwa namna ya kumlea mtoto na namna ya kutoa adhabu. Kwa hiyo, naamini kwamba tukidhibiti hili kupitia Bodi hii itatusaidia tuwe na walimu wazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini walimu wengine wamekuwa wakitembea na wanafunzi; anavaa jeans na t- shirt shuleni. Ukiuliza anakuuliza, kuna shida gani? Kwa hiyo, Wakuu wa Shule huko shuleni wamekuwa wakipata shida. Mkuu akimuuliza kwa nini unavaa jeans, t-shirt, nguo yenye maandishi mgongoni na kifuani, anauliza kuna tatizo gani, haelewi kwa nini anatakiwa asivae nguo hiyo kwa sababu amekosa maadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi siku hizi kwenye vyuo vyetu wanafunzi wamekuwa wakijifunza kusomea mitihani, kujifunza namna ya kujibu mitihani, lakini wakienda kazini, mambo wanayofanya ni tofauti kabisa na namna inavyotakiwa. Naamini kwamba Bodi hii itasimamia vizuri kuhakikishwa kwamba walimu wetu wanakuwa kwanza na maadili yanayotakiwa lakini pia wanayafuata ili watoto wetu waweze kujifunza kwao. Maana mwanafunzi huwa anajifunza kwa mwalimu. Sasa mwalimu akiwa wa hovyo, basi mwanafunzi anajifunza mambo ya hovyo hovyo na mwisho wa siku tunakuwa na Taifa lililo na mambo ya hovyo hovyo. Kwa hiyo, Bodi hii sasa itatusaidia kuhakikisha kwamba walimu wetu wanakuwa na maadili mazuri na hatimaye tutaanza kuwatengeneza Watanzania ambao wana maadili mazuri ya Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye kifungu cha 74(2) kinachoeleza kwamba walimu watapata usajili, kutakuwa na transitional provision ambayo itatolewa lakini haielezi vizuri. Labda pengine niseme mtakapotengeneza kanuni, mjaribu kuweka hasa kwenye ile fomu, kuwe kuna maoni ya Mkuu wa Shule ama Mwalimu Mkuu pale anapofundisha kwa sababu yule ndiye anayefanya assessment ya kwanza. Kwa hiyo, lazima atoe maoni kwamba huyu mwalimu aliyepo pale shuleni anafaa kuendelea kuwa mwalimu? Kuna walimu wapo huko, kwa mambo wanayoyafanya ni tofauti kabisa na mwalimu. Tusipokuwa na sehemu ambapo Mkuu wa Shule atamwangalia na kutoa maoni ya usajili wa huyu mwalimu kwamba asajiliwe au asisajiiwe kutokana na mwenendo wake akiwa pale shuleni, tutaendelea kuwa na walimu ambao hawana maadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, watakapotengeneza kanuni na kwenye fomu zile kuwe kuna sehemu ambapo Mkuu wa Taasisi kwa maana ya Mkuu wa Shule au Taasisi aweze kutoa maoni yake. Kupitia maoni hayo pia, yataweza kufikishwa hata kwa Afisa Elimu Kata au Wilaya ili wakitoa recommendation, huyu mwalimu aweze kupewa kibali. Tukitoa tu kwa sababu amelipa, tutaendelea kupata walimu ambao hawana maadili. Mimi naamini kwamba tukifanya hivyo tutakuwa na walimu wazuri na watasaidia kiwango cha elimu kiweze kupanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Bodi hii pia itatusaidia kutambua walimu kila mahali walipo. Kwa hiyo, kwa kuwa watakuwa wanasajili kila mwaka tutajua mwalimu fulani yuko wapi. Sasa hivi tuna uhaba wa masomo ya sayansi, kumbe kuna walimu wengine wako kwenye shule za binafsi wanafanya kazi huko, wanafundisha vizuri sana, kumbe tunaweza kuwachukua wale...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia. Ahsante sana.
Sheria ya Fedha ya Mwaka 2019
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa kupewa nafasi kuchangia kidogo Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2019, (The Finance Bill of 2019). Nianze kwanza kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na pia niipongeze Kamati kwa ushauri wao kwa Wizara na wameweza kuja na Sheria mpya nzuri ya Fedha ya mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nianze kidogo kuchangia kuhusu upande wa kuondoa ongezeko la thamani kwenye makasha ya majokofu ambayo yanatumika kwa ajili ya kuhifadhia matunda, maziwa, au mazao yanayotokana na hot culture na mazao ya nyama na mboga. Niipongeze sana Serikali, kwa sababu waliokuwa wanaathirika kutokana na hizi kodi za kulipia haya makasha ni wakulima na hawa wafanyabiashara wenye majokofu haya walikuwa wanaingiza gharama za majokofu, gharama za VAT kwenye bei ya mazao ambayo wanayauza wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa kufanya hivi, maana yake ni kwamba sasa mazao yao, kwa mfano kule kwetu tunazalisha maparachichi, mazao kwa mfano ya maparachichi, mazao ya mboga sasa, naamini kwamba bei itapanda kidogo kwa sababu baadhi ya gharama ambazo wafanyabiashara walikuwa wanaziingia, zimeweza kuondolewa. Kwa hiyo, hilo sasa ni wajibu wa Wizara kusimamia, kuhakikisha kwamba je, ni kweli baada ya kupunguza hiyo VAT, wakulima wamenufaika au bei zinabaki palepale. Kwa hiyo, hiyo ni muhimu sana kufuatilia ili tujue kama kupunguza huku kuna tija kwa wakulima au hakuna tija kwa wakulima wetu wa mazao haya ya mbogamboga, lakini pia wa mazao ya matunda.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze Serikali kwa kuondoa ushuru au kuongeza ushuru kwenye vifaa vya plastiki ambavyo vinatumika kutengenezea miundombinu vinavyotoka nje, hatua hii ni muhimu na niipongeze sana kwa sababu, ni kweli kwa kuwa nchini tumeanza kuzalisha vifaa hivi vya pastiki, mabomba ya plastiki na yanayotumika kutengenezea miundombinu kwa mfano ya maji, vipo viwanda vya kutosha. Mwanza wanazalisha, Dar es Salaam wanazalisha na tunaamini siyo muda mrefu na viwanda vingine vitaongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli visingeweza ku- compete na wenzetu wanaozalisha nje. Kwa hiyo, kuongeza hii tozo ya asilimia 10 maana yake tuna-discourage uingizaji wa hizi bidhaa toka nchi za nje na hatimaye tunaongeza wawekezaji wa ndani wawezwe kuzalisha vya kutosha, lakini pia tunaongeza fursa za ajira kwa vijana wetu kama ilivyoelezwa. Kwa hiyo, nipongeze sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha msingi sasa TBS ni muhimu sana kusimamia uzalishaji wa hizi bidhaa za mabomba, kwa sababu kama hawatasimamia vizuri na mwisho wa siku viwanda vikaanza kuzalisha mabomba ambayo hayaweze kustahimili, hayawezi kuwa na sifa stahiki, mwisho wa siku wananchi au wanaotaka kutengeneza miundombinu hii watarudi kulekule kununua kwenye nchi za wenzetu na hatimaye baadaye sisi wenyewe tutarudi sasa kuruhusu kurudisha hilo ongezeko, kupunguza bei.

Kwa hiyo, ili tuweze kulinda ni lazima na sisi sasa tusimamie, TBS wasimamie viwango vya uzalishaji, ubora wa haya mabomba yatakayokuwa yanazalishwa kwenye viwanda vyetu ili baadaye na sisi tuweze kuuza hata na nchi za nje kuliko kuendelea kuuza tu hapa ndani. Kwa hiyo, lazima tuwe na soko la nje, lakini pia tuwe na soko la ndani ili viwanda vyetu viwe endelevu na ajira ziweze kuongezeka kupitia hivi viwanda vya mabomba ya plastiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nipongeze kwa kurekebisha ile Sheria ya Usimamizi wa Kodi, Sura 438 ambayo sasa imeongeza kifungu kidogo ambacho kinaahirisha ulipaji wa kodi kwa mfanyabiashara au mtu anayeanzisha biashara au mwekezaji mara tu anapoanza biashara yake au anapoanza uwekezaji aanze kulipa kodi. Sasa amepewa miezi sita angalau kugharamia gharama nyingine kwa mfano, pango, leseni na vitu vingine ajipange kwa ajili ya kulipa kodi. Hatua hii nzuri sana na itawezesha wafanyabiashara sasa kujipanga vizuri na hatimaye kuweza kushiriki katika kulipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi wafanyabiashara wetu wamekuwa wanakwepa kulipa kodi pale wanapoanzisha biashara kwa sababu kwanza fedha nyingi wametumia kwenye mtaji wa uanzishaji wa biashara hiyo kwa maana ya chumba labda au eneo la kufanyia biashara na gharama nyingine lakini sasa kwa sababu hii kodi imeahirishwa kwa muda wa miezi wa sita wataweza kujipanga vizuri na hatimaye kulipa kodi stahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nipongeze hatua ya Wizara kwa kuondoa Kodi ya Ongezeko la Thamani kwenye mitambo hasa ya kuchimbia visima. Ni kweli hii ilikuwa inakwamisha sana uchimbaji wa visima kwenye maeneo mengi na tunasema kwamba Tanzania tunataka tumtue mwanamke ndoo kichwani lakini kwa kuwa kodi ilikuwa kubwa na vifaa hivi vilikuwa na VAT gharama za uchimbaji wa visima ilikuwa juu sana, utakuta ni shilingi milioni 20, shilingi 24 sasa Watanzania wengi hawawezi kumudu gharama hizo za uchimbaji wa visima, kwa hiyo, wengi walikuwa wanashindwa kuchimba visima. Kwa sababu mitambo hii sasa kodi itapunguzwa maana yake wataweza kununua mitambo hiyo na tunaamini kwamba maji katika maeneo yetu ya vijijini, mama zetu kule vijijini ambako mabomba ya kawaida au maji ya mtiririko na maji ya msukumo wa umeme hayawezi kufika basi sasa wataweza kuchimbiwa visima na hatimaye kupata maji na kuhakikisha kwamba mwanamke anatuliwa ndoo kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kidogo kuhusu kodi iliyowekwa kwenye bidhaa kama zile mawigi na nywele. Mimi ningesema kwamba sasa Serikali kwa nini mmeacha kuweka kwenye kucha maana wanawake wengi utakuta wanaweka kucha ndefu wanakuwa kama jini hivi, ingeongezwa kodi kwenye hayo mawigi, kucha na kope za bandia, mbaki hivi hivi, mnavaa mnapendeza mkiwa hivi hivi natural. Kwa hiyo, niwaombe sana pengine hizi kucha na kope za bandia nazo zingeongezwa kodi siyo mawigi tu peke yake. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa nafasi, ahsante sana. (Makofi/Kicheko)