Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Grace Victor Tendega (27 total)

MHE. RITTA E. KABATI (K.n.y. MHE. GRACE V. TENDEGA) aliuliza:-
Katika miaka ya 1990, Wilaya ya Iringa Vijijini kulikuwa na mradi wa usambazaji wa maji kwa kutumia chanzo cha maji ya Mto Mtitu ili kuondokana na adha ya maji inayowakumba wananchi wa Iringa Vijijini; juhudi za kufanya upembuzi yakinifu zilifanyika ili kuweza kusambaza maji kwa gravity kwenye vijiji vyote vya Kata za Maguliwa, Luhota, Mseke, Ifunda, Mgama na Maboga:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha mradi huu ili kuweza kuondoa tatizo la maji kwa wananchi wa Kata hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa kwa kushirikiana na Wizara ya Maji na Umwagiliaji, imepanga kufanya usanifu wa kina wa mradi mkubwa wa maji ambao utahusisha vijiji vya Kata za Ngawila, Luhota, Mseke, Ifunda, Mgama na Lugonga. Lengo ni kubaini uwezo wa chanzo cha Mto Mtitu katika kuhudumia maeneo hayo yote. Kazi hiyo imepangwa kufanyika katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, ambapo zimetengwa Shilingi milioni 49.5. Mradi huo utakapokamilika, jumla ya vijiji 17 vyenye wakazi wapatao 36,397 vitanufaika.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO (K.n.y MHE. GRACE V. TENDEGA) aliuliza:-
Mojawapo ya jukumu la Serikali katika kupambana na ugonjwa wa UKIMWI ni kuhakikisha wanatoa elimu kwa umma na waathirika kupatiwa huduma za matibabu kulingana na masharti ya Shirika la Afya Duniani (WHO) ambalo ndiyo hufadhili huduma hizo kwa takribani 100%.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba huduma hizo zinaendelea kutolewa hata kama msaada kutoka Shirika la Afya Duniani utatetereka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WATU WENYE ULEMAVU alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Grace Tendega, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha kwamba huduma za elimu kwa umma na matibabu kwa waathirika wa UKIMWI zinaendelea kutolewa hata pale misaada ya hisani itakapopungua, Serikali tayari imeanzisha Mfuko wa UKIMWI kupitia marekebisho ya Sheria ya UKIMWI Namba 6 ya mwaka 2015 kwa madhumuni ya kuratibu ukusanyaji fedha za kudhibiti UKIMWI nchini. Hata hivyo, Serikali kupitia Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016/2017 – 2020/2021) na bajeti za kila mwaka inaendelea kuhakikisha huduma kwa waishio na VVU na elimu kwa wananchi kuhusu UKIMWI inakuwa ajenda muhimu katika nchi yetu.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Tagamenda Substation ni kituo kikubwa kati ya vituo vinavyosafirisha umeme wa Gridi ya Taifa kwani kinapokea umeme kutoka Mtera, Kidatu na Kihansi, lakini vijiji vya Tagamenda, Ikuvilo na Wangama vinavyozunguka kituo hicho havina huduma ya umeme ingawa ndivyo vinalinda kituo hicho.
(a) Je, ni kwa nini Serikali inashindwa kutoa huduma
ya umeme katika vijiji vinavyozunguka kituo hicho?
(b) Je, ni sababu gani zinazofanya vijiji hivyo kukosa kupatiwa huduma hata ya umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Kitongoji cha Malulumo
Kijiji cha Tegamenda kiliwekwa katika Mpango wa kupatiwa umeme kupitia Shirika la Umeme TANESCO katika mwaka 2015/2016. Kazi hiyo ilianza Mei, 2016 na inakamilika Juni, 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za kupeleka umeme katika Kitongoji hicho zimejumuisha ujenzi wa njia ya msongo wa umeme wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa moja; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 1.4; ufungaji wa transfoma moja pamoja na kuwaunganishia umeme wateja 70. Kazi hii imekamilika kwa asilimia 90 na inagharimu shilingi bilioni 93.1.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa Mradi Kabambe wa Usambazaji Umeme Vijijini Awamu ya Tatu umeanza nchi nzima tangu mwezi Machi, 2017. Mradi huu utajumuisha vipengele-mradi vitatu vya densification, grid extension pamoja na off-grid renewable vinavyolenga kuongeza wigo wa umeme katika vijiji vyote nchini, vitongoji vyote vilivyobaki, taasisi za umma na maeneo ya pembezoni ambayo hayajafikiwa na miundombinu ya umeme ikiwa ni pamoja na visiwa. Vijiji vya Ivukilo, Wangama pamoja na maeneo mengine ya kijiji cha Tagamenda vimewekwa katika utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya Tatu wa Densification na Grid Extenson utakaokamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 10.3; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 9.7; ufungaji wa transfoma tatu pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 300. Gharama ya kazi hii ni shilingi bilioni 14.45.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Upembuzi yakinifu wa kutumia chanzo cha maji cha Mto Ibofwe ili kumaliza tatizo la maji katika Kata za Magulilwa, Luhota, Mseke, Ifunda, Mgama na Maboga ulifanyika kati ya mwaka 1995 – 2000 chini ya usimamizi wa Mbunge wakati huo, Mheshimiwa George Mlawa na bajeti ya utekelezaji wake kupitishwa na Bunge hili ili uwe katika kipindi cha mwaka 2000-2005/2005-2010.
Je, ni tatizo gani lililofanya mradi huo usikamilike na kuwaacha wananchi wakiendelea kuteseka wakati Bunge lilikwishapitisha bajeti ya mradi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji wa kutumia chanzo cha Mto Ibofwe ulifanyiwa usanifu wa awali miaka ya 1990 lakini haukufanyiwa usanifu wa kina (detailed design) ambao ungebaini mahitaji na gharama halisi za kutengeneza mradi huo ndiyo maana haukutekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuwapatia huduma ya maji wananchi wa Kata za Maboga, Lumuli, Isupilo na Itengulinyi, Serikali inatekeleza mradi mkubwa wa maji unaogharimu shilingi bilioni 2.18 utakaonufaisha wakazi 6,914 katika maeneo hayo. Mradi huo ulioanza kutekelezwa mwaka 2013/2014 ulisimama utekelezaji wake mwaka 2015 kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 umetengewa shilingi milioni 800 na unatarajiwa kukamilika Desemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kati ya Julai 2016 na Desemba 2017, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo imechimba visima sita katika Kata za Magulilo kisima kimoja, Luhota visima vitatu, Maboga kisima kimoja na Mgama kisima kimoja vinavyohudumia wananchi 1,600. Idadi ya visima kwenye kata hizo tangu miaka ya 1990 hadi sasa imefikia visima 41 vinavyohudumia wakazi 8,200.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mwaka huu 2017/2018, jumla ya shilingi 410,000,000 zimetengwa kutekeleza miradi ya maji ya Izazi - Mnadani, Migoli - Mtera, Malinzanga, Isupilo – Lumweli – Itengulinyi - Magunga na Mfyome. Mpango wa muda mrefu wa Serikali ni kufanya usanifu wa kina (detailed design) ili hatimaye tutumie chanzo cha Mto Ibofwe kumaliza kabisa matatizo ya maji kwenye maeneo hayo. Usanifu wa kina utafanyika mwaka 2018/2019 kwa gharama ya shilingi milioni 49.56 ambazo ziko kwenye mapendekezo ya bajeti ya mwaka 2018/2019 endapo Bunge litaridhia.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Kuna uhaba wa nyumba za kuishi walimu licha ya juhudi za wananchi kujenga nyumba za walimu wa shule za msingi na sekondari; walimu hao pia wanahitaji kujenga nyumba zao wenyewe za kudumu.
Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu wa kutoa mikopo kwa walimu ili wajenge nyumba zao binafsi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa upo uhaba wa nyumba za walimu katika shule za msingi na sekondari ndiyo maana imekuwa ikijitahidi kila mwaka kujenga nyumba za walimu. Katika mwaka huu wa fedha 2017/2018 Serikali kwa kushirikiana na wananchi, imekamilisha ujenzi wa nyumba 274 za walimu na hivyo kufikisha idadi ya nyumba 14,640 kati ya nyumba 67,711 zinazohitajika kwenye shule za sekondari. Aidha, nyumba 290 za walimu zimejengwa kwenye shule za msingi na hivyo kufikisha idadi ya nyumba 45,638 kati ya nyumba 175,930 zinazohitajika. Takwimu hizo zinabainisha kwamba familia za walimu 52,071 katika shule za sekondari na familia za walimu 130,300 kwenye shule za msingi zinaishi kwenye nyumba za kupanga au nyumba zao binafsi. Ni wazi kwamba mahitaji ya nyumba za walimu ni makubwa mno.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imedhamiria kuendelea kuweka kipaumbele cha kujenga nyumba za walimu za kuishi familia mbili, nne au sita ambazo ni za gharama nafuu kulinganisha na gharama za kujenga nyumba za kuishi familia moja. Kipaumbele cha juu kitaendelea kuwekwa kwenye maeneo yenye mazingira magumu ya kupata nyumba za kupanga hasa maeneo ya vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa mikopo kwa ajili ya Walimu kujenga nyumba zao binafsi ni kama ulivyo kwa watumishi wengine wa Serikali, ambapo mtumishi anaruhusiwa kukopa kwenye taasisi au benki yenye mkataba maalum na mwajiri kwa kujaza fomu ili akatwe marejesho ya mkopo kutoka kwenye mshahara ambapo makato ya mkopo hayatakiwi kuzidi theluthi mbili ya mshahara na mkopo wote kulipwa kwa kipindi cha kati ya miezi 36 (miaka mitatu) hadi miezi 300 (miaka 25) kulingana na masharti ya taasisi husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa taasisi zinazotoa mikopo ya nyumba kwa watumishi wa Serikali wakiwemo walimu ni Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Kampuni ya Nyumba za Watumishi (Watumishi Housing Company), Benki ya Afrika (Bank of Africa – BOA) kupitia mpango wake wa WEZESHA, mabenki kadhaa mengine kama NMB, CRDB, Azania na kadhalika na kampuni nyingine kama vile T-Mortgage yanayolenga zaidi kuwakopesha watumishi wa kipato cha chini na cha kati.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili watumishi wakiwemo walimu wapate mikopo ya kujenga nyumba binafsi kwenye maeneo watakayochagua wao, inatakiwa Wakurugenzi wa Halmashauri wawasiliane na taasisi zinazokopesha ili waingie makubaliano maalum yatakayowawezesha watumishi wa Halmashauri wanaotaka mikopo ya kujenga nyumba binafsi wakiwemo walimu kupata mkopo.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Katika nchi yetu kuna kampuni za simu zenye ushindani mkubwa lakini katika Jimbo la Kilolo, hasa maeneo ya Kimala, Kidabaga, hayana mawasiliano ya simu:-
Je, ni lini Serikali itazishawishi kampuni za simu kusimika minara yao kwenye maeneo ambayo hayana mtandao wa mawasiliano ya simu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASIALIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa, Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote iliainisha Kata ya Kimala na Kidabaga kwa ajili ya kupelekewa huduma za mawasiliano kupitia Kampuni ya Mawasiliano ya Halotel. Tayari Halotel imejenga mnara eneo la Kimala na mnara huo umeanza kutoa huduma tangu tarehe 17 Septemba, 2016. Halotel ni kampuni pekee inayotoa huduma za mawasiliano katika eneo hilo la Kimala. Vilevile Halotel imejenga mnara katika eneo la Kidabaga ambao pia, umeanza kutoa huduma tangu tarehe 9 Mei, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana wakati swali hili linaletwa na Mheshimiwa Mbunge, labda siku hiyo kulikuwa hakuna mawasiliano eneo hilo, lakini kuna barua ambayo nimeletewa na Mbunge wa Jimbo la Kilolo, Mheshimiwa Venance Mwamoto, ambayo inaeleza maeneo tofauti kabisa ambayo hayana mawasiliano tofauti na aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge. Hata hivyo, Wizara itawatuma wataalam wake kwenda kuangalia maeneo hayo kama kuna changamoto yoyote ili tuangalie uwezekano wa kuongeza coverage katika maeneo hayo.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. GRACE V. TENDEGA) aliuliza:-
Kesi za dawa za kulevya na upelelezi vimekuwa vikichukua muda mrefu sana na kusababisha wakati mwingine ushahidi kupotea na watuhumiwa kuachwa huru baada ya upelelezi kukamilika:-
Je, kwa nini Serikali isianzishe Mahakama za Dawa za Kulevya kwenye Viwanja vya Ndege, Bandari na mipakani ili watuhumiwa wafikishwe Mahakamani punde tu ushahidi ukiwa mikononi kama zifanyavyo nchi nyingine ikiwemo India?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba wa Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uanzishwaji wa mahakama katika kushughulikia aina fulani ya makosa, ni suala la kisheria linalohitaji ushirikishwaji mkubwa wa wadau wote husika wa haki jinai (criminal justice). Kwa kutambua hilo, Serikali imeshaanza mazungumzo ya awali na wadau hao wa haki jinai, ukiwemo mhimili wa Mahakama ili kuona uwezekano wa kusikiliza mashauri ya watuhumiwa wa dawa za kulevya wanaokamatwa katika maeneo ya viwanja vya ndege, bandarini na maeneo mengine ya mipaka ya nchi, kwa kutumia Mahakama zinazotembea (mobile courts).
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wawe na subira wakati Serikali ikijadiliana na wadau wa haki jinai kuhusiana na suala hilo.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Sera ya Afya imebainisha makundi yenye msamaha wa matibabu ambayo ni wazee kuanzia miaka 60 na kuendelea, watoto chini ya miaka 5, watoto wanaoishi na TB na UKIMWI:-

Je, ni lini Serikali itaweka Watu wenye Ulemavu kuwa miongoni mwa watu wanaohitaji msamaha wa gharama za matibabu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mhesimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imefanya mapitio ya Sera ya Afya ya mwaka 2007 na kuandaa mapendekezo ya Sera mpya ya Afya. Katika mapitio ya Sera ya Afya ya mwaka 2007 changamoto mbalimbali za matibabu kwa makundi ya msamaha ziliibuliwa na watoa huduma pamoja na watumiaji huduma hizo. Moja ya changamoto iliyojitokeza ni hospitali zetu kuwa na wagonjwa wengi wa msamaha na hivyo kushindwa kuboresha huduma za afya. Kutokana na changamoto hiyo ya kuwa na makundi mengi ya msamaha, Wizara iliona ni vyema ikaboresha utaratibu wa msamaha kwa kuhakikisha kuwa watu wasio na uwezo tu ndiyo wanaopatiwa msamaha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mapendekezo ya Sera mpya na Afya kila mwananchi mwenye uwezo atapaswa kugharamia huduma za afya. Sera pendekezwa inaainisha njia mahsusi zitakazowezesha Serikali kubaini wananchi wote wenye uwezo ili waweze kuchangia gharama kabla ya kupokea huduma, kwani ni wazi kuwa si kila mlemavu ana kipato duni. Hivyo, wananchi watakaothibitika katika maeneo yao kuwa hawana uwezo wa kuchangia wakiwemo walemavu wataendelea kupatiwa matibabu bila kuchangia gharama za matibabu. Aidha, Serikali inatambua changamoto ya uchangiaji wa huduma za afya na inaandaa utaratibu wa bima ya afya kwa Watanzania wote ikiwa ni pamoja na kundi la walemavu.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo watoto wengi njiti huzaliwa na akinamama wanaojifungua watoto hao njiti wengi wao ni waajiriwa ambao hupata changamoto ya likizo ya uzazi inayotosha kwa malezi ya awali ya watoto hao njiti:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha akinamama hao wanaongezewa likizo ya uzazi?

(b) Akinamama hao wanapojifungua pia, hupata changamoto ya vifaa kama vile vifaa vya kukamulia maziwa, dawa na gharama za matibabu; Je, Serikali imejipangaje kuwasaidia gharama za vifaa hivyo?

(c) Je, Serikali ina mpango gani wa kudumu wa kutokomeza suala la akinamama kuzaa watoto njiti?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Kazi ya Mwaka 2004, iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2015 inaelekeza kuwa mama aliyejifungua mtoto mmoja apewe likizo ya malipo ya siku 84 na siku 100 kwa mama aliyejifungua watoo pacha, sheria hiyo pia imeweka wazi kuwa mama anayenyonyesha anatakiwa kupewa saa mbili kwa siku, ili apate muda wa kunyonyesha. Serikali haina muda wa kuongeza muda wa likizo ya uzazi kwa sasa.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kutekeleza sera ya Afya ya Mwaka 2007 ya Kutoa Huduma Bila Maipo kwa Makundi Maalum wakiwepo akinama wajawazito na mwongozo wa uchangiaji unaeleza wazi kuwa, kundi hili halipaswi kugharamia huduma za afya pale wanapohitaji. Hivyo, basi, Wizara inafanya juhudi kubwa katika kuboresha huduma kwa akinamama wajawazito, hususan, wanapojifungua kwa kutumia njia mbalimbali. Kwa sasa Wizara inatekeleza Mpango wa Pili wa kuboresha afya ya uzazi na mtoto, yaani One Plan II ya mwaka 2016 mpaka 2020 ambapo imeweka vipaumbele mahususi vya kuboresha afya ya watoto wachanga ikiwemo watoto njiti nchini. Kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 Wizara imetenga fedha bilioni 22.5 kwa ajili ya huduma ya mama wajawazito na katika Mwaka wa Fedha 2019/2020 inatarajia kuomba idhini ya Bunge kutumia fedha kiasi cha bilioni 29.5 kwa ajili ya kundi hili na hivyo hakuna akinamama wanaojifungua wanaoripotiwa kukosa huduma za dawa na vifaa tiba kabla na baada ya kujifungua katika vituo vya Serikali.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kujikita katoka afua mbalimbali kwa lengo la kudhibiti visababishi vya kuzaliwa watoto njiti, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha akinamama wajawazito wanaanza kliniki mapema mara tu wanapohizi kuwa na ujauzito, kuhudhuria kliniki ipasavyo, ili kuchunguza na kutibiwa magonjwa mbalimbali, ikiwa yatabainika kwa kuzingatia vilevile ushauri wa lishe n.k. Afua nyingingine zinazolenga kuokoa maisha ya watoto wachanga kama vile uanzishwaji wa vyumba maalum vya matunzo na matibabu ya watoto wachanga, kwa maana ya neonatal care units, sambamba na upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, kwa ajili ya watoto wachanga ikiwemo watoto njiti.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Wakati akiwaapisha Wakuu wa Mikoa tarehe 15/03/2016 Mhe. Rais alitoa agizo la kuwakamata vijana wote watakaokutwa wakicheza mchezo wa “pool table” na kuwapeleka kambini wakalime:-

(a) Je, Serikali imeandaa kambi ngapi na kujua huduma za kujikimu kwa vijana hao wakati watakapokuwa wakiendelea na shughuli za kilimo na kipindi cha kusubiri mavuno yao?

(b) Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kupunguza tatizo la ajira kwa vijana ili kuondokana na wimbi la vijana kuzurura na kushinda bila kufanya kazi?

(c) Je, Serikali imefanya sensa na kujua ni vijana wangapi wanaofanya kazi usiku na kupumzika mchana au mchana na kupumzika usiku ili kubaini wazururaji wa mchana na wanaocheza “pool table” mchana kwa sababu ya kukosa ajira?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, msingi wa agizo la Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano Dkt. John Pombe Magufuli kuzuia vijana kucheza “pool table” wakati wa kazi umelenga kusisitiza na kuimarisha dhana na tabia ya kila mwenye uwezo wa kufanya kazi anafanya kazi katika sekta mbalimbali za kiuchumi ili kuchangia kukuza pato la Taifa na kupunguza umaskini. Katika kuhakikisha kwamba vijana wanashiriki kwenye shughuli za kiuchumi, Serikali kupitia Tawala za Mikoa na Wilaya imetenga maeneo maalum ya uzalishaji mali kwa vijana ambapo jumla ya ekari 217,882 zimeelekezwa katika kukidhi mahitaji ya shughuli za kilimo, ufugaji, viwanda na biashara ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwepo wa Vituo vya Maendeleo ya Vijana na Majengo ya Viwanda “Industrial Sheds” umesaidia kuwapa mafunzo vijana na kuwajengea uwezo wa kuongeza thamani katika mazao ya kilimo.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na tatizo la ukosefu wa ajira kuwa vijana, Serikali imeendelea kutekeleza mikakati ifuatayo:-

(i) Kuwajengea vijana ujuzi kupitia Programu ya Kukuza Ujuzi Nchini ili vijana kutumia ujuzi wa mafunzo mbalimbali kujiajiri na kuajiri vijana wengine. Kwa mwaka huu wa fedha, Serikali inatekeleza mafunzo ya stadi mbalimbali za kazi ambapo jumla ya vijana 49,265 watanufaika.

(ii) Kuweka mazingira bora ya uwekezaji nchini ili kuvutia uwekezaji mkubwa kwenye sekta zenye uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira hususani kilimo, ufugaji, madini na viwanda.

(iii) Utekelezaji wa dhana ya local content katika miradi mikubwa ya kimkakati ya Serikali katika maeneo ya uchukuzi, nishati na miundombinu ya barabara na reli.

(iv) Kuwezesha vikundi vya vijana kupitia zabuni za manunuzi ya ndani kwenye kila Halmashauri za Manispaa na Wilaya nchini Tanzania kupitia Akaunti Maalum kama mabadiliko ya mwaka 2016 ya Sheria ya PPRA yanavyoelekeza.

(v) Uwezeshwaji kiuchumi kwa vijana kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na mikopo ya asilimia 10 za mapato ya ndani ya Halmashauri.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imelipokea wazo la kujua vijana wanaofanya kazi usiku na wanaofanya kazi mchana. Hivyo suala hili litawasilishwa katika Mamlaka ya Takwimu ili lizingatiwe katika sensa ya watu na makazi itakayofanyika mwaka 2022.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA (K.n.y. MHE. GRACE V. TENDEGA) aliuliza:-

Walimu wenye weledi wa kuwafundisha Watu Wenye Ulemavu ni wachache sana nchini.

Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha Walimu hao ni wa kutosha?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA (K.n.y. WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA) alijibu:-

Mheshimimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekonolojia napenda kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimimiwa Spika, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na changamoto ya upungufu wa Walimu wenye taaluma ya Elimu Maalum. Changamoto hii ina sababishwa na ongezeko la uandikishaji wa wanafunzi wenye ulemavu kutokana na mabadiliko chanya ya kimtazamo na uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa elimu kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimimiwa Spika, mahitaji ya Walimu wa Elimu Maalum nchini ni Walimu 8,882 katika shule maalum na vitengo vinavyopokea wanafunzi wenye mahitaji maalum 706. Hadi kufikia Disemba 2018 Walimu 5,556 wenye taalum ya Elimu Maalum ngazi za Astashahada, Stashahada na Shahada walihitimu katika Vyuo mbalimbali nchini vikiwemo Chuo cha Ualimu Patandi na Chuo Kikuu Dodoma.

Mheshimimiwa Spika, Serikali imekamilika upanuzi wa Chuo cha Ualimu Patandi ili kukiongezea uwezo wa kudahili. Pia Chuo kimeanzisha kozi ya Elimu Maalum katika ngazi ya Astashahada kwa Walimu tarajali kwa mwaka wa masomo 2018/2019. Hatua hii itaongeza idadi ya Walimu wanaojiunga na mafunzo ya Ualimu wa Elimu Maalum ili kupunguza changamoto ya Walimu wenye taaluma ya Elimu Maalum wanaohitajika nchini.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Watu wenye ulemavu wamekuwa wakipata adha kubwa katika kupata matibabu ikiwemo kukosa fedha kwa ajili ya matibabu:-

Je, ni lini Serikali itahakikisha inawapatia bima ya afya watu wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara imefanya mapitio ya Sera ya Afya ya mwaka 2007 na kuandaa mapendekezo ya Sera mpya ya Afya. Katika mapitio ya Sera ya Afya ya Mwaka 2007, changamoto mbalimbali za matibabu kwa makundi ya msamaha ziliibuliwa na watoa huduma pamoja na watumiaji wa huduma hizo. Moja ya changamoto iliyojitokeza ni hospitali zetu kuwa na wagonjwa wengi wa misamaha na hivyo kushindwa kuboresha huduma za afya. Kutokana na changamoto hiyo ya kuwa na makundi mengi ya msamaha, Wizara iliona ni vyema ikaboresha utaratibu wa misamaha kwa kuhakikisha kuwa wananchi wasio na uwezo tu ndio wanaopatiwa msamaha.

Mheshimiwa Spika, katika mapendekezo ya Sera mpya ya Afya kila mwananchi mwenye uwezo atapaswa kugharamia huduma za afya. Sera pendekezwa inaainisha njia mahsusi zitakazowezesha Serikali kubaini wananchi wote wenye uwezo ili waweze kuchangia gharama kabla ya kupokea huduma, kwani ni wazi kuwa si kila mlemavu ana kipato duni. Hivyo, wananchi watakaothibitika katika maeneo yao kuwa hawana uwezo wa kuchangia ikiwemo walemavu, wataendelea kupatiwa matibabu bila kuchangia gharama za matibabu.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali inatambua changamoto za uchangiaji wa huduma za afya na inaandaa utaratibu wa bima ya afya kwa Watanzania wote ikiwa ni pamoja na kundi la walemavu.
MHE. GRACE V. TENDEGA Aliuliza:-

Akina mama wajawazito wamekuwa wakitozwa fedha kuanzia shilingi 50,000/= hadi 70,000/= wasipojifungulia katika Vituo vya Afya hasa katika Jimbo la Kalenga; huku vituo hivyo vikiwa mbali na maeneo wanayoishi.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga maeneo ya kusubiri kujifungua katika Vituo vya Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, majengo ya wajawazito kujisubiria yanalenga kupunguza umbali kwa wajawazito kufika kwenye vituo vya huduma za afya pindi wanapokaribia kujifungua. Lengo likiwa ni kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga vinavyosababishwa na umbali kutoka katika vituo vya kutolea huduma.

Meshimiwa Spika, katika kutatua changamoto hii, Serikali imeendelea kujenga vituo vya huduma za afya kote nchini na kujenga Hospitali za Halmashauri 102, Vituo vya Afya 487 na Zahanati 1,198 katika kipindi cha Novemba, 2015 hadi Septemba, 2020. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali za Halmashauri 67; shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali 67 za Halmashauri na shilingi bilioni 27 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali mpya za Halmashauri. Kiasi cha shilingi bilioni 27.5 pia kimetengwa kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati 555.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mpango wa ujenzi na ukarabati wa Vituo vya Afya nchini kote, umepunguza umbali kwa wananchi kuvifikia vituo vya huduma za afya na hivyo viashiria vya huduma na vifo vya wajawazito vimepungua kutoka 11,000 mwaka 2015 hadi 3,000 mwaka 2020. Serikali itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya huduma za afya kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Barabara za kutoka Kata ya Kalenga kuelekea kata za Ulanda, Maboga, Wasa, Kihanga hadi Kijiji cha Mwambao ni mbovu sana: -

Je, ni lini Serikali itahakikisha barabara hizi zinapitika hata kwa kiwango cha changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2019/ 2020 Serikali kupitia TARURA katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ilichonga tuta la barabara lenye kilometa 25 iliyozinufaisha Kata za Maboga, Wasa na Kalenga kwa gharama ya Shilingi milioni153. Vile vile TARURA ilifanya matengenezo ya kawaida kwenye barabara ya Magubike, Igangindung’u yenye urefu wa kilomita nane iliyovinufaisha Vijiji vya Kihanga na Mwambao kwa gharama ya Shilingi milioni 69.17. Katika mwaka wa fedha 2021 barabara hizo zimetengewa kiasi cha Shilingi milioni 54 kwa ajili ya matengenezo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya barabara na madaraja nchi nzima kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Kumekuwa na changamoto ya huduma za Afya katika Zahanati zetu hasa ukosefu wa dawa pamoja na huduma bure kwa wazee, watoto na akinamama wajawazito.

Je, ni lini Serikali itahakikisha Sera ya Afya inatekelezwa bila tatizo lolote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini kwa kuongeza bajeti ya dawa, vitendanishi na vifaa tiba kutoka shilingi bilioni 31 katika mwaka wa fedha 2015/2016 hadi shilingi bilioni 270 katika mwaka wa fedha 2020/2021. Ongezeko hilo la fedha limewezesha kuongeza upatikanaji wa dawa muhimu (tracer medicine) kutoka wastani wa asilimia 31 mwaka 2015/2016 hadi asilimia 90 kufikia Aprili 30, 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia Mei, 2021 Serikali imetoa huduma ya matibabu bila malipo yenye gharama ya shilingi bilioni 30.1 kwa wananchi wa makundi maalum milioni 12 ikijumlisha wazee, wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi, bado kuna changamoto ya upatikanaji wa baadhi ya dawa za makundi maalum kama wazee, wajawazito na watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano. Ili kukabiliana na changamoto hiyo, mwezi Novemba, 2020 Serikali ilitoa shilingi bilioni 41.2, mwezi Februari, 2021 Serikali ilipeleka shilingi bilioni
18.2 katika vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi kwa ajili ya ununuzi wa dawa na mwezi Mei, 2021 Serikali imepeleka shilingi bilioni 80 na kufanya jumla ya fedha zote zilizopelekwa kwa ajili ya dawa kufikia shilingi bilioni 140.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuboresha upatikanaji wa dawa na bidhaa nyingine za afya ili kuboresha huduma kwa makundi maalum na wananchi kwa ujumla.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA K.n.y. MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Suala la Vitambulisho vya ujasiriamali limekuwa ni changamoto hasa kwa Wafanyabiashara ambao wana mitaji midogo.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha au kufuta vitambulisho hivyo?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Machi 2019, Serikali kwa kuwathamini na kuwajali wajasiriamali na watoa huduma wadogo ilianzisha utaratibu wa vitambulisho ili kuwawezesha kufanya biashara katika mazingira bora na tulivu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba kweli kuna changamoto zilizojitokeza katika utoaji wa vitambulisho kwa wajasiriamali na watoa huduma wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais -TAMISEMI imefanya tathmini ya zoezi zima la ugawaji, usajili na matumizi ya vitambulisho vya wwajasiriamali na watoa huduma wadogo katika mikoa na halmashauri ili kubaini changamoto zilizopo na kufanya maboresho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia mwaka 2021 vitambulisho hivyo vimefanyiwa maboresho kadhaa ikiwemo kuwekwa picha na jina la mjasiriamali mdogo aliyepatiwa kitambulisho pamoja na ukomo wa muda wa kutumika kitambulisho hicho ambao ni mwaka mmoja tangu tarehe ya kupatiwa kitambulisho badala ya mwaka wa kalenda kama ilivyokuwa awali.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Umeme wa REA kama ilivyoahidi katika Vijiji vya Kitayawa, Kipera, Lupalama, Itagutwa, Ikungwe na Lyamgungwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Kipera, Itagutwa, Ikungwe, Lupalama na Lyamgungwe vimepata umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Kwanza. Kazi iliyobaki ni kufikisha umeme katika vitongoji vya vijiji hivyo vilivyobaki bila umeme katika miradi ya ujazilizi (densification) kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO imeshapeleka umeme katika Kitongoji cha Kitayawa ambacho kipo katika Kijiji cha Tagamenda Kata ya Luhota, Wilaya ya Iringa. Aidha, TANESCO pamoja na REA wanaendelea kuunganisha umeme kwa wateja wa Kitongoji cha Kitayawa na vitongoji vingine vya Jimbo la Iringa Mjini na Iringa kwa ujumla kadri ya upatikanaji wa fedha. (Makofi)
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, ni kwa nini Serikali iliamua kujiondoa kwenye mpango wa uendeshaji wa Serikali kwa uwazi wakati silaha kubwa ya kupambana na rushwa ni uwazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, uamuzi wa Serikali kujitoa OGP haujaathiri uendeshaji wa Serikali kwa uwazi kwa kuzingatia ukweli kwamba Serikali inao utaratibu wa ndani wa kuhakikisha kuwa kunakuwepo na uendeshaji wa shughuli za Serikali kwa uwazi wakati wote kwa kuwa na vyombo na taasisi zilizokasimiwa majukumu ya kusimamia na kufuatilia Sera ya Uwazi na Uwajibikaji. Mfano, TAKUKURU, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na Tume ya Utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kujiunga na OGP ni hiari kwa nchi mwanachama na vilevile inaweza kujitoa kwa hiari. Kwa msingi huo Serikali iliamua kujitoa kwa hiari.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ngazi za kimataifa, Serikali imeendelea kuwa moja ya nchi zilizoridhia mfumo wa kukaguana wa nchi za kiafrika APRM (African Peer Review Mechanism) ambao ulianzishwa mwaka 2003 na Kamati ya Wakuu wa Nchi za Kiafrika.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itazigawa upya Halmashauri nchini ili Wananchi wapate huduma kwa urahisi kutokana na jiografia za Halmashauri hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikigawa maeneo mapya ua Utawala zikiwemo Halmashauri kwa lengo la kusogeza huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa, Serikali inaendelea na ujenzi wa miundombinu ya huduma na kiutawala katika mamlaka mpya ambazo hazina miundombinu hiyo muhimu ili kuziwezesha kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa jumla ya majengo ya utawala 109 yenye thamani ya shilingi bilioni 356.8 yanaendelea kujengwa kote nchini, lengo la Serikali kwa sasa ni kukamilisha miundombinu katika mamlaka zilizopo kabla ya kuanzisha mamlaka mpya, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO K.n.y. MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, ni vigezo gani vinapaswa vifuatwe na halmashauri ili fedha za maendeleo ziweze kutolewa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa fedha za maendeleo zilizotengwa katika bajeti hutolewa kwa halmashauri kwa kuzingatia Waraka na Mwongozo wa Wizara ya Fedha na Mipango kila mwaka kwa kuzingatia maelekezo ya Kifungu Na. 5 cha Kanuni za Sheria ya Bajeti Sura 439, Kifungu cha 6 cha Sheria ya Fedha za Umma, Sura 348 na Kifungu cha 12 cha Sheria ya Bajeti Sura 439.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya vigezo hivyo ni pamoja na halmashauri kuwasilisha maombi ya fedha za utekelezaji ikionesha utayari wa kuanza kutekeleza mradi mara baada ya kupokea fedha. Ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, Serikali ipo tayari kuondoa kodi kwenye vifaa vinavyotumiwa na Watu wenye Ulemavu wakati wa kuingia nchini?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetoa msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), SURA 148 na ushuru wa forodha kwenye vifaa vilivyotengenezwa mahsusi kwa ajili ya Watu Wenye Ulemavu. Msamaha wa VAT umeainishwa katika kipengele cha 8 na 12(d) cha Jedwali lililopo kwenye Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani, Sura ya 148.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa vilivyopewa msamaha wa kodi ni pamoja na baiskeli na magari yaliyotengenezwa mahususi kwa matumizi ya watu wenye ulemavu. Vile vile, Serikali imetoa msamaha wa VAT kwenye huduma za elimu zinazotolewa katika vituo vya mafunzo ya mwili na akili kwa watu wenye ulemavu, ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, lini Serikali itamaliza kujenga Mradi wa Maji katika Vijiji vya Sawala, Mtwango, Rufuna na Kibao vilivyopo Mufindi Kusini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Tendega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji katika Kata ya Mtwango, na miradi imekamilika kwenye Vijiji vya Sawala na Mtwango. Kwa sasa miradi inaendelea katika Vijiji vya Rufuna na Kibao ambapo utekelezaji umefikia asilimia 52. Kazi zinazoendelea ni pamoja na ulazaji wa mabomba umbali wa Kilometa 21, ujenzi wa matenki mawili yenye jumla ya ujazo wa lita 450,000 na vituo 21 vya kuchotea maji. Utekelezaji wa kazi hizo utakamilika mwezi Julai, 2023 na wananchi kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inapata data za bidhaa zote za kilimo zinazosafirishwa nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea kuboresha mfumo wa Agricultural Trade Management Information System (ATMIS) kwa ajili ya kuufungamanisha na mfumo wa pamoja wa forodha wa Tanzania (Tanzania Custom Intergrated Systems - TANCIS) wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Kufunganishwa kwa mfumo wa ATMIS na TANCIS kutaboresha upatikanaji wa takwimu za mazao na bidhaa za kilimo zinazoingizwa au zinazosafirishwa nje ya nchi.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, watalii wangapi walitembelea Mbuga ya Ruaha kwa mwaka 2019/2020 na upi mkakati wa kuongeza watalii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasilinna Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2019/2020 Hifadhi ya Taifa ya Ruaha ilipokea jumla ya watalii 18,678 ambapo watalii 11,601 kutoka nje ya nchi na watalii 7,077 kutoka ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha idadi ya watalii inaongezeka, Serikali imeweka mikakati ifuatayo: -

(i) Kuanzisha na kuboresha miundombinu ya barabara za ndani ya hifadhi kwa kiwango cha changarawe na kuboresha barabara kuu kutoka Iringa Mjini hadi hifadhini.

(ii) Kuongeza na kuboresha viwanja vya ndege saba ndani ya hifadhi.

(iii) Kuongeza miundombinu ya malazi kwa kuongeza vitanda 263 na kutangaza maeneo ya uwekezaji.

(iv) Kuongeza na kuboresha mazao ya utalii kama utalii wa puto, boti, farasi, kuvua samaki, utalii wa kitamaduni na kihistoria, utalii wa mikutano na utalii wa michezo.

(v) Kuongeza utangazaji wa vivutio vya hifadhi katika masoko ya ndani na nje ya nchi.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, kwa nini Serikali haipeleki fedha za maendeleo kwa wakati katika Halmashauri nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa wakati, mfano hadi kufikia mwezi Mei, 2023 kiasi cha shilingi trilioni 1.08 sawa na 116% zilipelekwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini kote.

Mheshimiwa Spika, miradi inayotekelezwa na wakandarasi fedha hutolewa kulingana na hati ya madai ya kazi kulingana na utekelezaji wa majukumu hayo. Aidha, kwa miradi Iinayofanywa na force account, fedha hutolewa kwa kuzingatia utayari wa Halmashauri wa kuanza utekelezaji wa miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, ufafanuzi wa taratibu hizi unatolewa kulingana kwa mujibu wa kanuni na mwongozo wa utoaji fedha katika utekelezaji wa bajeti za Serikali ya mwaka 2021 iliyotolewa na Wizara ya Fedha na Mipango.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Je, kuna mkakati gani wa kutenga fedha ili kuweka uwiano sawa kwa bajeti za Halmashauri kwani Halmashauri nyingi haziwezi kujiendesha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua utofauti uliopo wa uwezo wa Halmashauri kujiendesha baina ya Halmashauri moja na nyingine kutokana na uwezo wa ukusanyaji wa mapato ya ndani ya Halmashauri. Kwa kutambua hilo, Serikali imeziweka Halmashauri kwenye madaraja manne kwa kuzingatia uwezo wa Halmashauri kukusanya mapato kutokana na fursa za vyanzo vya mapato vilivyopo kwenye eneo husika la utawala.

Mheshimiwa Spika, ili kuziwezesha Halmashauri zisizo na fursa za kukusanya mapato makubwa kujiendesha na kwa kuzingatia madaraja hayo Serikali imechukua hatua zifuatazo:-

(i) Kuzipunguzia viwango vya upelekaji wa fedha za mapato ya ndani kwenye miradi ya maendeleo;

(ii) Kuziondolea mchango wa asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi wa Barabara;

(iii) Kuzisaidia kulipa stahiki za Viongozi hususan Wakurugenzi na Wakuu wa Idara;

(iv) Kuzisaidia kulipa posho za kila mwezi za Waheshimiwa Madiwani; na

(v) Kuziongezea viwango vya ruzuku ya matumizi ya kawaida na ruzuku ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuziwezesha Halmashauri zenye uwezo mdogo wa ukusanyaji wa mapato ili ziweze kujiendesha.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Maafisa Masuuli na Wahasibu katika Halmashauri wanapata mafunzo juu ya uandaaji wa taarifa za fedha za mwisho za halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetoa mafunzo kwa jumla ya watumishi 210 juu ya uandaaji wa taarifa za fedha za mwaka unaoishia tarehe 30 Juni, 2022. Mafunzo hayo yametolewa kwa watumishi waliopo ngazi ya mikoa na halmashauri zote nchini.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha Mwongozo wa Uhasibu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wa mwaka 2020 (Local Authority Accounting Manual) na Waraka wa Ufungaji Hesabu kila mwaka. Maboresho hayo yanakusudia kuzikumbusha taasisi za umma juu ya mambo ya msingi ya kuzingatia na kuwaongoza Maafisa Masuuli na Wahasibu katika kutekeleza majukumu yao ikiwa ni pamoja na uandaaji wa hesabu za mwisho.