Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Richard Mganga Ndassa (58 total)

MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pia nishukuru kwa majibu ya utangulizi, lakini naomba tu kuiambia Serikali kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa ajili ya uchumi pamoja na kijamii. Pia niseme barabara hii ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne na wakati barabara hii inaahidiwa na Rais wa Awamu ya Nne, Rais wa sasa Dkt. John Pombe Magufuli alikuwepo. Sasa hili suala la upembuzi yakinifu, ni lini hasa kwa sababu swali hapa la msingi, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami kwa kuzingatia kwamba hii ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna nilivyomwelewa, anasisitiza tu kwamba hii kazi ya upembuzi yakinifu ikamilike haraka ili ahadi ya Marais wetu, Rais wa Awamu ya Nne na Rais wa Awamu ya Tano wakati alipokuwa Waziri wa Wizara ya Ujenzi itekelezwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua nafasi hii kumthibitishia kwamba Wizara yetu itatekeleza ahadi hiyo kikamilifu.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ninaomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, kwa sababu hapa Tanzania tunayo mazao makuu ya biashara, ambayo yalikuwa yanajulikana katika kuongeza uchumi wa nchi yetu ambayo ni pamba, kahawa, korosho pamoja na katani.
Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba mazao haya ambayo yalikuwa yanatoa ajira kubwa, uchumi kwa nchi yetu, kwamba mazao haya sasa yanatafutiwa soko lenye uhakika hasa pamba ambayo zaidi ya Mikoa 14, Wilaya 42 zilikuwa zinategemea zao la pamba, Serikali ina mpango gani hasa? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Ndassa, Mbunge wa Sumve kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana kwa kazi yake nzuri ya Ubunge aliyoifanya na Wabunge wengi wapya tuige kwake, maana yake Mheshimiwa Ndassa ameaminiwa na wananchi wake kwa muda mrefu kwa ajili ya kufanya kazi nzuri namna hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango mzuri sana wa kuendeleza mazao yote ya biashara, mpango wa kwanza ambao Serikali imeweka uzito mkubwa ni kuanzia kwenye ubora wa zao, kwa sababu ubora wa zao una uhusiano wa moja kwa moja na upatikanaji soko lake.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili ambalo Serikali imeweka mkazo mtasikia hata kwenye Mpango utakapowasilishwa na Dkt. Mpango muda siyo mrefu, imeweka mkazo kwenye kuongeza thamani ya mazao, kwa sababu na yenyewe ni hatua nzuri unapoenda kwenye kupata soko la zao husika na baada ya hapo tukishaongeza thamani kwa kupitia viwanda tutakuwa na uhakika wa kuweza kuuza mazao yanayotokana na mazao yetu ya biashara kwa bei ambayo itawaletea manufaa wanachi wetu na kuweza kuwafanikisha kuweza kuchochea watu wengi kujihusisha na uzalishaji wa mazao hayo kwa sababu yatakuwa na tija.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza naomba niipongeze sana Serikali kwa kazi nzuri sana inayofanya ya kusambaza umeme kupitia REA, REA I, REA II na REA III kwa sasa. Swali langu kwa sababu kuna vishoka wamejitokeza ambao wanaharibu sifa nzuri ya TANESCO, wanaojifanya kwenda kutandaza nyaya kwenye nyumba za watu lakini wanachukua pesa zao halafu hawa hawarudi tena kwa ajili ya kusambaza huo umeme. Je, Serikali inaweza ikawaagiza Mameneja wa Kanda, Mameneja wa Mikoa, Mameneja wa Wilaya ili kusudi waende wawabaini hao vishoka wasiwaibie wananchi hasa katika Jimbo la Sumve?
NAIBU WAZIRI NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kati ya wahudumu wanaotoa huduma kwenye Shirika la Umeme kuna wafanyakazi wengine wala siyo wa TANESCO ni wafanyakazi bandia ambao wanaitwa vishoka. Pamoja na Wabunge mnaonisikiliza nichukue nafasi hii tu kuwatahadharisha kwamba wafanyakazi wa Mashirika ya Umeme Tanzania ni wafanyakazi ambao wanafanyakazi kwa maadili ya utumishi wa umma. Hata hivyo, tunatambua inawezekana wapo wachache kati yao ambao pia wanashirikiana na vishoka kuhujumu nguvu umeme ya TANESCO.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi tumechukua hatua makusudi tumeanza kuwabaini wale Mameneja ambao wanashirikiana na vishoka tumeshaanza kuwa-identify na mpaka sasa kuna vishoka takribani 19 wamekamatwa na naomba sana nitamke hili na kuanzia sasa ofisi zetu zote za Kanda pamoja na Mikoa wale Makandarasi wanaohusika kuunganisha nyaya kwenye nyumba wanaorodheshwa kwenye ofisi zetu.
Kwa hivyo basi, kama kutakuwa na wakandarasi ambao hawapo kwenye orodha ya ofisi zetu hao ni vishoka na hawakubaliki. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, niongeze kwenye jibu hilo, hadi sasa Shirika la Umeme TANESCO limeshaanza kuchukua hatua kwa watumishi wake wasio waadilifu, hadi sasa watumishi 12 wamesimamishwa kazi kwa sababu ya kuhujumu miundombinu ya TANESCO pamoja na kushiriki kwenye kuwaunganishia umeme watu kwa njia ya vishoka.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimwulize Mheshimiwa Waziri kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ahadi ya Serikali na Waziri mwenyewe humu Bungeni aliwaahidi Watanzania kwamba Miradi ya REA II itakamilika yote Juni, 2015; siyo mara moja wala mara mbili; ni sababu ipi iliyopelekea miradi hii kutokukamilika kama Mheshimiwa Waziri alivyosema? (Makofi)
La pili, kwa sababu huyu Mkandarasi mara kwa mara amekuwa akiwachangisha Watanzania shilingi 200,000/= au shilingi 300,000/= kwa kila nguzo ya umeme wale wanaohitaji; Serikali inatoa tamko gani ili kusudi wananchi hao wapate huduma hii kama ilivyotarajiwa? (Makofi)
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba tulikusudia kwamba ikifika Juni, 2015 miradi iwe imekamilika, lakini tuwe na ukweli wa kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Pato letu la Taifa ni karibu dola bilioni 53 na mwaka jana tulikuwa na uchaguzi, tulikuwa na Katiba, uchumi wetu hauna uzito wa kukabili vitu vikubwa kwa wakati mmoja. (Makofi)

WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, huo ni ukweli wa kifedha na kiuchumi. Kwa hiyo, ndiyo maana sasa Serikali imemaliza majukumu makubwa fedha zinaenda REA, kwa hiyo, miradi itakamilika kama ilivyopangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile napenda kuongezea kwamba miradi ya REA na Miradi yote ya umeme, ndugu zangu Watanzania inahitaji fedha nyingine za kutoka nje. Kwa hiyo, sisi Wizara tumeanza kutafuta fedha kutoka nje. Kwa mfano, Tanzania ndiyo iliwakilisha Afrika kuweka hizi taratibu za umeme kwa kila raia wa sayari hii (Sustainable Energy for All 2030). Ni sisi ndiyo tuliwakilisha Bara la Afrika na tutahakikisha sisi ndiyo tutapata fedha nyingi kutoka huko na tumeishaanza kuzipokea. Kwa hiyo, miradi itaenda kwa kasi kubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la Chico, tumewaambia Wakandarasi kwamba endapo pataonekana kuna rushwa, adhabu kubwa kabisa ni kwamba huyo mkandarasi hatapata miradi mingine ya REA. Kwa hiyo, kama huyu mkandarasi anachangisha, ni kwamba na wiki ijayo tunafanya tathmini adhabu yake nyepesi sana ni kutopata mradi wowote wa REA kuanzia mwaka huu.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza naomba nisahishe jina langu hapa inasomeka Ngassa, siyo Ngassa ni Ndassa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maelezo mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini naomba Serikali itambue kwamba suala la maji ni suala kila Mtanzania, kila mwananchi anahitaji maji na ndiyo maana unaona Wabunge wote wanasema kuhusu maji.
(a) Swali langu, kwa sababu Serikali katika mwaka 2000 na 2004 iliamua, maamuzi magumu yenye tija, kuyatoa maji ya Ziwa Victoria kuyapeleka Kahama, Shinyanga. Je, Serikali ina mpango gani mrefu wa kupeleka maji ya Ziwa Victoria katika Mikoa tisa ili maji hayo yawanufaishe Watanzania na mikoa hiyo ni Mwanza, Mara, Kagera, Simiyu, Singida na Dodoma. Serikali ina mpango gani kwa sababu mahitaji ya maji ni makubwa na maji ya Ziwa Victoria yapo hayana kazi nyingine. Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kuhakikisha kwamba maji yanafika katika maeneo hayo?
(b) Mheshimiwa Waziri wa Maji, wananchi wa Jimbo la Sumve katika Kata ya Nkalalo na Mabomba wanashida kubwa ya maji, naomba nikuombe pamoja na maelezo haya utembelee tuende ukajionee mwenyewe jinsi wananchi wa Tanzania wa Jimbo la Sumve wanavyopata taabu ya maji katika Jimbo langu.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimezungumza jana kwamba tumeleta mapendekezo ya mwongozo kwa kutengeneza mpango wa miaka 2016/2017 na nilisema katika sekta ya maji tumetoa ahadi kwamba katika miji yote ya Mikoa inayozungukiwa na Ziwa Victoria tutahakikisha tunachukua maji ya kutosha kuyafikisha kwenye maeneo husika kwa kiwango ambacho tumeshasema kwenye Ilani, kwamba Miji Mikuu ya Mikoa ipate asilimia 95 ikifika 2020 na ipate asilimia 100 ikifika 2025.
Kwa hiyo, naomba nilihakikishie Bunge hili kwamba azma hiyo ambayo pia Mheshimiwa Rais wetu ameahidi tutakwenda kufanya, tutaomba Waheshimiwa Wabunge muweze kutuunga mkono katika kupanua vyanzo vya upatikanaji wa fedha hasa kuongeza Mfuko wa Maji ili tuweze kutekeleza miradi yote hii ambayo kila Mbunge ameomba Serikali iweze kufanya, ahsante. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa, Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua kwamba itakuwa ni Serikali ya viwanda, je, Selikali ina mpango gani wa kuanza kufufua viwanda hivi ambavyo vilikufa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Kiwanda cha Chai cha Mponde kilichoko katika Wilaya ya Lushoto, Jimbo la Bumbuli, kimefungwa kwa takribani miaka mitatu sasa na mpaka sasa hakijaanza uzalishaji. Mara ya mwisho wakati Msajili wa Hazina anakuja pale alituambia kwamba zimeandaliwa shilingi bilioni nne kwa ajili ya kuanzisha shughuli za uzalishaji na kwenye randama ya Wizara ya Fedha na Wizara ya Viwanda na Biashara fedha hiyo hatujaiona. Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusu kufunguliwa kwa kiwanda hiki?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Shangazi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa Serikali imedhamiria kujenga viwanda na hasa kuanzia viwanda vidogo sana, viwanda vidogo, viwanda vya kati pamoja na viwanda vikubwa. Mikakati ambayo Serikali inaichukuwa kwa sasa ni pamoja na kutengeneza mazingira wezeshi ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ili kuwawezesha Watanzania kuwekeza zaidi. Mkakati wa pili ni kufanya utafiti hasa kwa viwanda ambavyo vimedhoofika au vimekufa ili kuviweka katika mazingira mazuri ili kutafuta wawekezaji wengine kwa ajili ya kuviendeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo, nimhakikishie Mheshimiwa Shangazi tu kwamba Serikali inafanya mikakati mingine ya ziada ikiwa ni pamoja na kutoa mikopo kama mnavyoona kwamba Serikali itatoa mikopo shilingi milioni 50 kila kijiji ili kuwawezesha Watanzania waweze kufanya pia biashara kuendesha viwanda vidogo vidogo. Pamoja na hayo, Serikali imeweka mazingira ya kisera na kisheria ili kuhakikisha kwamba sasa tasnia ya viwanda inaimarishwa zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusiana na Kiwanda cha Chai cha Lushoto, ni kweli kabisa kiwanda hiki kimedhoofu na siyo Lushoto tu, viwanda vingi vimekufa sehemu mbalimbali. Mkakati wa Serikali uliopo ni kuhakikisha kwamba inatafuta wawekezaji binafsi ili waweze kujadiliana na wenye kiwanda hicho ili wawekezaji hao waweze kukiimarisha Kiwanda cha Lushoto na kianze kufanya kazi kama kawaida.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri, Halmashauri zinatofautiana kimapato na Kituo cha Afya cha Nyambiti hakina gari, ni utaratibu gani sasa utumike ili kituo hiki kiweze kupata gari kwa sababu uwezo ni mdogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la upatikanaji wa gari katika vituo vya afya, tulipokuwa tunapitia mchakato wa bajeti yetu ya mwaka huu 2016/2017, tulikuwa tukifanya analysis ya halmashauri mbalimbali katika suala zima la sekta ya afya, kila halmashauri iliweka kipaumbele chake. Kuna wengine waliweka kipaumbele cha ujenzi wa miundombinu, kwa mfano kwa ndugu yangu pale zahanati aliyosema ya Chiwale, wametenga karibuni milioni 287 kwa ajili ya kituo kile cha afya. Wengine kipaumbele chao walichoweka ni ununuzi wa gari la wagonjwa. Kwa hiyo, vipaumbele hivi vinatofautiana kati ya zahanati na zahanati.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumjulisha Mheshimiwa Ndassa kwa sababu sijajua kipaumbele walichoweka katika eneo hili, sisi na wenzetu wa Wizara ya Afya tutaangalia katika bajeti ya mwaka huu tumegusa vipi katika eneo hilo. Mwisho wa siku ni kwamba, lazima kwa umoja wetu wote tuangalie jinsi gani tutafanya maeneo kama hayo ambayo wananchi wanapata shida waweze kupata fursa za kuwa na gari la wagonjwa ili mama akipata matatizo aweze kupelekwa hospitali ya karibu kupata huduma. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ndassa naomba tulichukue hili tujadiliane kwa pamoja na kuangalia bajeti yenu ya halmashauri mlipanga vipi kama vipaumbele vyenu vya awali.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mwanza hapo awali kulikuwa na zaidi vinu 15 vya kuchambulia pamba, kikiwepo na cha Nyambiti Ginnery, Ngasamo. Mheshimiwa Waziri kwa sababu nilishaongea na Mheshimiwa Waziri Marehemu Abdallah Kigoda, pia niliongea na Waziri aliyekuwepo wakati huo Mheshimiwa Mama Nagu; ni lini sasa angalau Nyambiti Ginnery iweze kutengeneza pamba nyuzi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndassa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pamba limekuwa na hoja kubwa kwenye bajeti yangu, majibu niliyotoa ni kwamba tarehe 02 Mei, nilizindua mkakati namna ya kuboresha pamba kusudi iendane na ujenzi wa uchumi wa viwanda. Ijumaa mikoa yote inayolima pamba, tunakutana Mwanza na mimi nitakuwepo niwapitishe kwenye mkakati na nitahakikisha kwamba Kiwanda cha Nyambiti kiweze kuingizwa katika mchakato wa kuchambua pamba na kutengeneza kiwanda ikiwezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo siku ya Ijumaa shughuli nzima inafanyika Mwanza mimi nitakuwepo pale, tuchambue suala la pamba ili ule mkakati wangu wa nguo uweze kutekekezwa.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Katika maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba ruzuku ya pembejeo pia inapelekwa kwenye zao la pamba. Mheshimiwa Waziri unajua kwamba mpaka leo hakuna ruzuku yoyote inayopelekwa kwenye zao la pamba, kwenye mbolea pamoja na mbegu?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia ruzuku katika zao la pamba linatolewa kwa utaratibu tofauti na ule unaotolewa katika mahindi na mpunga. Kwenye zao la pamba ruzuku inatolewa katika mbegu, kwa hiyo, niko tayari kuongea na Mheshimiwa Mbunge tujaribu kupitia yale ambayo yeye anayafahamu kuhusu hili lakini nimfahamishe tu kwamba kuna ruzuku inatolewa lakini ni katika utaratibu ambao ni tofauti kidogo. Kama nilivyosema mazao mengine kama kahawa, korosho vilevile ruzuku inatolewa lakini mara nyingi ni kwa kupitia mifuko maalum ambayo imeundwa kwa ajili ya mazao hayo. Lakini niko tayari kuongea naye tuangalie kuhusu hili.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri kwamba, nakumbuka ulifanya ziara mkoani Mwanza na ulizungumza na wadau wa pamba. Msimu wa pamba umeanza Jumatatu, bei elekezi tunaambiwa ni shilingi 1,000, lakini wapo wanunuzi wengine wanasema hawawezi kununua pamba kwa bei ya shilingi 1,000.
Je, nini msimamo wa Serikali kuhusu bei ya pamba, kwa sababu viwanda vyote hivyo Manonga, MWATEX, vinahitaji pamba ya kutosha; na ili wakulima wa zao la pamba waweze kulima zaidi lazima bei iwe nzuri, nini msimamo wa Serikali kuhusu bei ya pamba?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UFUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, sheria ya zao la pamba inataka bei elekezi itajwe na Bodi ya Pamba kwa kushauriana na wakulima, wanunuzi na wadau wengine wa zao lenyewe. Hiyo processes ilifanyika na hatimaye Bodi ya Pamba ikatangaza bei elekezi ya shilingi 1,000 kwa kilo moja pamba mbegu. Sasa wanunuzi wanayo hiari ya kupima wenyewe, kama hiyo bei wakinunua kwa bei hiyo elekezi au zaidi ya pale, watakuwa na faida katika biashara yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimuarifu Mheshimiwa Mbunge, kwamba hadi hapa ninapozungumza makampuni nane, yamekwisha pewa license ya kununua pamba, na ununuzi wa pamba umeanza. Utaratibu wa msimu wa pamba ni mrefu kidogo, kwa hivyo kwa miaka ya nyuma msimu unapoanza kampuni hizi huwa zinaendelea kupata leseni na kuongezeka kadri msimu unavyokwenda mbele. Kwa hivyo, bei ya pamba ya sasa ni nzuri kwa wakulima, pia baada ya bodi kupitia vizuri ile mjengeko wenyewe wa bei, wana hakika pia itakuwa na manufaa hata kwa wanunuzi wa pamba.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimwulize Mheshimiwa Waziri, kwa sababu Wakala wa Madini (TMAA) wanafanya kazi nzuri sana. Mwaka 2010 na mpaka mwaka 2015 waliweza kukamata madini yenye thamani ya Dola bilioni mbili, lakini pia kwa upande wa shilingi, jumla ya shilingi bilioni 64 zilikamatwa. Je, kwa utaratibu huo huo Serikali ina mpango gani wa kuzuia wachimbaji katika migodi hasa katika usafirishaji wa ule mchanga kwenda kupimwa nje?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli kabisa sasa hivi mchanga wote wa concentrate, yaani copper concentrate na hasa unaotoka kwenye mgodi mkubwa wa Bulyanhulu unasafirishwa kwenda ama China ama Japani. Sababu kubwa ya kufanya hivyo ni kwa sababu hapa viwanda vya kuchenjua dhahabu na kuachanisha madini, havijajengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia namwambie Mheshimiwa Ndassa, ni kweli kabisa uwekezaji huu unahitaji mitaji mikubwa; na siyo chini ya Dola 1,000 kuanzisha mradi wa kuchenjua madini hapa nchini. Hata hivyo, kama Serikali, tunatambua sana mchango wa TMAA mamlaka yetu. Kweli kabisa kwa kutumia TMAA imedhibiti asilimia kubwa sana ya upotevu wa madini ambao ulikuwa unatokea hapo nyuma.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimkumbushe tu Mheshimiwa Ndassa kwamba ni kweli, mwaka 2015, migodi mikubwa kama GGM ililipa shilingi milioni 117 kama dola kwa ajili ya royalty. Hii kutokana na kazi ya TMAA. Pia local levy iliyolipwa ni dola bilioni 4.7 za Marekani, hiyo ni kutokana na udhibiti wa TMAA.
Kwa hiyo, Serikali tunaendelea sasa kuangalia uwezekano wa kuhamasisha wawekezaji wakubwa kuanza sasa kujenga viwanda vya kuchenjua dhahabu hapa nchini. Hata hivyo, itachukua muda, bado Serikali tunalifanyia kazi. Hii ni kwa sababu inahitaji mitaji mikubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, wazo la Mheshimiwa Ndassa tumelichukua, tutalifanyia kazi kama ambavyo Mheshimiwa Ndassa tunashirikiana, tunakushukuru sana.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. TBC na Radio ya Taifa ndiyo visemeo vya Serikali. Je, wakati mnaboresha mitambo, Serikali ina utaratibu gani wa kuwapeleka wafanyakazi wa TBC na Radio ya Taifa kwenda nje kujifunza ili kusudi waendane na teknolojia ya sasa, kuwapeleka nje kwenda kusoma?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Ndassa kwa kazi nzuri anayofanya ya kutetea tasnia ya habari kwa sababu na yeye mwenyewe ana background ya habari. Pili TBC imekuwa na mipango mizuri ya kuwapeleka wafanyakazi wake kwenda kuongeza ujuzi wao nje ya nchi, lakini pia na kuwaalika Wataalam mbalimbali kuja hapa kwa ajili ya kuongeza ujuzi wao. Mfano mzuri, wenzetu wa China wamekuwa wakitusaidia sana, wafanyakazi wengi wanakwenda kujifunza. Hata hivi tunapoongea wako wafanyakazi ambao wanaongeza ujuzi wao China, lakini tunao Wachina ambao wako hapa kupitia ushirikiano wa TBC na Star Times, nao wanaongeza ujuzi wa watu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaamini program hizi zitaendelea na tutaendelea kuziboresha mara kwa mara ili wafanyakazi wetu waendane na kasi ya mabadiliko ya teknolojia duniani.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, kwa sababu kazi ya ujenzi wa zahanati ni kazi nyingine, ujenzi wa vituo vya afya ni kazi nyingine, upelekaji wa tiba ni kazi nyingine. Je, Serikali kwa sababu inajua kwamba upo upungufu mkubwa sana wa wataalam katika ngazi zote, imejipanga namna gani kuhakikisha kwamba zahanati na vituo vyote vile vinakuwa na waganga wa kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya mpango wa Serikali tumezungumza hapa. Ni kweli tunajenga structures hizi lakini lazima tupeleke vifaa tiba, dawa na wataalam. Hili tumelizungumza na mlikuwa mnajua tulikuwa na mchakato katika suala zima la ajira, lakini kutokana na changamoto ya watumishi hewa, maelekezo yametoka ya kumaliza kufanya analysis ya kuangalia watumishi hewa na baadaye tutaendelea na mchakato wa kupata ajira mpya na vijana wetu watapata kazi katika maeneo ya site.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninamuomba Mheshimiwa Ndassa, tuwe na subira, jambo hili linakwenda vizuri, kwa sababu vijana wanaopakuliwa kutoka vyuoni, utaratibu wa Serikali utakapokaa vizuri sasa watapelekwa maeneo husika baada ya kupata ajira ili wakawapatie wananchi huduma ya afya.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Miji ya Sumve, Nyamatala, Malya, Nyambiti, Hungumarwa inakua kwa kasi sana. Mheshimiwa Waziri katika ziara yake aliyoifanya Kwimba nilimuomba vitendea kazi kama gari na vifaa vya kupimia. Nataka kujua ombi letu hilo limefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nilitembelea kwenye Jimbo lake na hayo anayoyasema tuliyazungumza. Kikubwa ambacho nataka nimhakikishie, katika bajeti yetu ambayo imepitishwa na hata kwenye bajeti ya Wizara ya Fedha ambayo tunaendelea kuijadili, kuna fedha kiasi cha shilingi bilioni 8.8 zimetengwa kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji kwa sababu tatizo la upimaji ni tatizo kubwa katika nchi yetu na tunasema eneo lililopimiwa ni asilimia 15 tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pale ambapo tutakuwa tumefanikiwa kupata pesa hizo baada ya kuwa tumepitisha bajeti hii tunajua hizo shilingi bilioni 8.8 kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji ziko pale. Tukishapata, vifaa hivyo vitakwenda katika Kanda. Jimbo la Sumve liko kwenye Kanda ya Ziwa, kwa maana hiyo, eneo la Kanda wakipata vifaa hivyo basi upimaji katika maeneo ya Nyamatala na mengine aliyoyasema yatafanyiwa upimaji kwa wakati muda utakapofika.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mwaka 2013 Serikali ilitenga jumla ya shilingi bilioni 3.6 kwa ajili ya kuchimba visima vinane katika vijiji vinane, lakini hadi sasa shilingi milioni 184 tu zilizopelekwa.
Naiuliza Serikali ni lini sasa kwa sababu azma ya Serikali ilikuwa ni kuchimba visima vinane; ni lini sasa Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya visima hivyo?

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, ujasikia vizuri swali? Mheshimiwa Ndassa sehemu ya mwisho ya swali ni lini?
MHE. RICHARD M. NDASSA: Katika Jimbo la Sumve na Jimbo la Kwimba Serikali ilipanga kuchimba visima vinane katika vijiji vinane vya Isunga, Kadashi, Gumangubo, Shilima, Mande na Izimba A. Fedha zilizotengwa ni shilingi bilioni 3.6 lakini hadi juzi ni shilingi milioni 185 tu ndizo zilizopelekwa, kwa hiyo, miradi hii imekwama, ni lini sasa Serikali imepeleka fedha hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, tumeishaelekeza tayari, kwamba ukishapata bajeti, Halmashauri ikipata bajeti, kitu cha kwanza ni kufanya taratibu za manunuzi. Kuhakikisha kwamba mkandarasi anaanza kazi, na akishatekeleza kazi utuletee hati, ya madai ya mkandarasi tuweze kuipeleka kwa Waziri wa Fedha aweze kutupatia fedha.
Nina wasiwasi lakini tutashirikiana na Mheshimiwa Ndassa kuangalia ni kazi ipi imeishafanyika tangu kupeleka hiyo hela, inawezekana kwa sababu hata wakati wa ziara yangu niliona hiyo. Unakuta mtu ametengewa bajeti lakini hajafanya kazi yoyote, anasubiri kwamba kwanza aletewe hela, utaratibu huo kwa sasa hatunao. Ukishapata bajeti basi fanya taratibu za manunuzi na mkandarasi afanye kazi akifanya kazi ndio tutampatia hela.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, tarehe 11/10/2014 ilikuwa siku ya Jumamosi saa 5.32; Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne wakiwa na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, walizindua daraja la Mto Simiyu kule Maligisu na kuahidi kwamba mita 50 kuingia kwenye daraja na mita 50 kutoka kwenye daraja itawekewa lami. sasa nataka kujua, je, ahadi hii ya Mheshimiwa Rais itatekelezwa lini?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Richard Ndassa ni Mwalimu wangu. Naomba nimhakikishie kama ambavyo nimekuwa nikiongea naye kabla kwamba maungio haya ya daraja la Mto Simiyu kama ambavyo Viongozi wetu waliahidi, tutahakikisha tunayatekeleza. Naomba tu aendelee kutukumbusha, kwa kadri hapa ninavyoongea, wahusika wote kuanzia TANROAD Mkoa wa Simiyu, pamoja na Makao Makuu, wananisikia. Tuhakikishe hili daraja pamoja na barabara yake ambayo iliahidiwa, tuifanyie kazi kama ambavyo viongozi wetu waliahidi.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri swali la nyongeza. REA Awamu ya II imebakiza siku 27, je, wameshafanya tathmini ya kutosha nchi nzima? Kama jibu ni ndiyo utekelezaji wake ni asilimia ngapi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nachagua swali la tathmini ya ujumla. Nimhakikishie Mheshimiwa Ndassa na nimshukuru tumeshirikiana, mpaka sasa tathmini tuliyofanya ukamilifu wa kazi ya REA Awamu ya II ni asilimia 91 ya kazi zote zilizokwishakamilika.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Wizara hii inashughulika na habari, utamaduni, sanaa na michezo. Kwa idhini
yako, naomba uniruhusu niulize swali la michezo. Timu yetu ya vijana under 17
imebahatika kwenda kwenye fainali itakayofanyika Gabon Aprili, ni mwezi
mmoja tu sasa umebaki. Je, Serikali pamoja na TFF tunajiandaa namna gani ili
timu yetu hii isiende kushiriki bali iende kushindana na kuleta ushindi katika nchi
yetu?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu
Spika, ni kweli kwamba Serengeti Boys wamefanya vizuri sana katika mchezo wa
mpira wa miguu katika nchi yetu na kuiletea heshima nchi yetu. Nichukue nafasi
hii kuwapongeza kwa moyo wao wa dhati ambapo wamejitahidi kupambana
na kwa kweli wanafanya vizuri. Kama Serikali, kwanza nilihakikishie Bunge lako
kwamba tumeshiriki kikamilifu kwa wao Serengeti Boys kufanikiwa kufika pale
walipofika ikiwemo kutafuta rasilimali kwa wadau. Niwashukuru sana wadau wa
sekta binafsi ambao wamekuwa wakijitolea kuhakikisha timu yetu hii inafanya
vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kwa kushirikiana na TFF tumejipanga
kwamba Serengeti Boys watakwenda kupiga kambi ya mwezi mzima kabla ya
kwenda kwenye fainali za mashindano haya. Serikali ikishirikiana na wadau wa
sekta binafsi, tutahakikisha zinapatikana rasilimali za kutosha kuhakikisha vijana
hawa wanapiga kambi yao, lakini pia wanakwenda kuchukua kombe na siyo
kushiriki. Kila tukiangalia uwezekano wa kushinda, ni mkubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge na
Watanzania kwa pamoja tuungane pamoja kwa dua zetu na rasilimali zetu
kuhakikisha kwamba Serengeti Boys wanakwenda na wanarudi na ushindi hapa
nchini.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante sana, naomba nimuulize bwana Waziri; katika Wilaya ya Kwimba kuna vijiji kumi ambavyo vilipangiwa kupelekewa maji katika mradi wa vijiji kumi, zaidi ya miaka kumi leo,
naomba leo nijue katika hivi vijiji vya Kadashi, Isunga, Shirima na Mhande mkandarasi hayupo site mpaka leo na kwa sababu nilishafanya mawasiliano na Mheshimiwa Waziri wa Maji mwenyewe kwa muda mwingi, nataka leo anipe majibi kazi hii ya miradi hii ya maji katika Wilaya ya Sumve na Kwimba lini itakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli anachokisema Mheshimiwa Mbunge haongopi na mimi naomba nikiri kwamba nimefika Jimboni kwake kule na miongoni mwa jambo katika taarifa ambayo niliyosomewa ni changamoto ya maji na hali kadhalika suala zima la vijiji kumi katika suala zima la mpango wa World Bank na ni kwa sababu nimesema hapa nyuma kwamba miradi hii ya maji maeneo mengi sana ilisimama na ilisimama kwa sababu hapa nyuma suala zima la kifedha lilikuwa siyo zuri zaidi, lakini
sasa hivi Serikali katika Mfuko wa Maji tumejipanga vizuri kuhakikisha miradi hii inatekelezeka. Lakini jambo lingine utakuta kuna changamoto ya mkandarasi, kwa hiyo kwa sababu taarifa zimeshakuja Serikalini na Waziri wa Maji taarifa hii anayo sasa kwa kina basi nadhani mpango mzuri utafanywa naamini jambo hili
litafanyika vizuri na miradi hii itakamilika na wananchi wa Jimbo lako watapata maji kwa sababu commitment ya Serikali hii kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa sababu tunao uwanja wetu wa Taifa (Dar es Salaam) ambao ni wa kimataifa na ili kuutangaza uwanja huo, na ili kutangaza utalii na kuongeza ajira kwa nini Serikali sasa isije na mpango wa kuziomba Balozi zetu nje ili timu zao za Taifa huko ziliko zije kuutumia uwanja wetu wa mpira wa uwanja wa Taifa, na wakimaliza kucheza mpira au baada ya kucheza mpira wachezaji hao waende kwenye hifadhi zetu ili watangaze utalii wa nchi yetu kupitia uwanja wa Taifa?
NAIBU WAZIRI, HABARI UTAMADUNI SANAA NA
MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, wazo lake ni zuri, tumelichukua na tutakwenda kulifanyia kazi na tutarejesha majibu, ahsante sana.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Matatizo yaliyopo Mbozi Vwawa yanafanana sana na Kituo cha Afya cha Malya. Kituo cha Afya cha Malya kinahudumia Maswa, Malampaka na Kwimba. Kwa sababu Kituo cha Afya cha Malya kwa sasa kimezidiwa, miundombinu ya majengo na vyumba vya kusaidia wazazi havitoshi, Serikali ina mpango gani sasa wa kuwekeza angalau adha zilizopo pale ziweze kupungua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, hii sehemu ya Kwimba ina Majimbo mawili, Jimbo la Mheshimiwa Ndassa na Mbunge mwingine lakini ukiangalia hospitali yetu ya wilaya na kule anakosema Malya ni kweli. Ndiyo maana naomba nimshukuru Mheshimiwa Mbunge, katika initiative zake za kutusumbua mimi na Waziri wa Afya alileta Kituo hiki cha Afya cha Malya kiweze kupewa kipaumbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi TAMISEMI tumeshapitisha bajeti yetu na Wizara ya Afya imeshapitisha yao ni kwamba sasa hivi tunaenda kufanya uwekezaji mkubwa katika Kituo cha Afya cha Malya. Naomba nimhakikishie kwamba ombi lake kama Wizara ya Afya na Wizara ya TAMISEMI tumelichukua, tunaenda kufanya ukarabati mkubwa. Katika vile vituo 100 na Malya ni kimojawapo, tunaenda kuwasaidia wananchi wa jimbo lake.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. TASAF awamu ya pili ilianzisha mradi wa barabara ya Bungurwa-Msunga; leo ni zaidi ya miaka 10 na yapo makalvati yapo tayari zaidi ya 50. Je, ni lini sasa mradi huo au ujenzi wa barabara hiyo utatekelezwa?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kama nitakuwa nimemsikia vizuri; ni kwamba kuna mradi wa makalvati ambao ulikuwa haujamalizika na anataka kufahamu ni lini labda utatekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nipende tu kusema kwamba, tulipotekeleza TASAF awamu ya kwanza na awamu ya pili ni kweli iko miradi ambayo haikuweza kukamilika. Hata hivyo kwa maelekezo ambayo Serikali iliyatoa; tulitoa maelekezo kwa halmashauri zetu kuhakikisha kwamba wanaorodhesha miradi yote ambayo walikuwa hawajatekeleza au imeanza kutekelezwa lakini haijakamilika waweze kutengea fedha katika bajeti ili iweze kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge tutafuatilia mradi huo wa kalvati katika Kata ya Misungwi ili tuone ni hatua gani imefikiwa ili mradi huo uweze kukamilika mapema.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali ilitenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya Mradi wa Maji Sumve, Madya na Malampaka, mwaka 2017/2018 ilitenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya mradi huo. Sasa Mheshimiwa Waziri katika majibu yake, kwa sababu ili maji yafike Mji wa Malampaka ni lazima yafike Sumve na Malya. Sasa nataka kujua, tulitegemea kwamba ungetaja, angalau kwamba Serikali imetenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya mradi huo, lakini hukutaja hata kidogo. Sasa swali Mheshimiwa Waziri, pesa zilizotengwa sasa hivi hazipo tena au mradi huo umeshakufa?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, majibu niliyoyatoa haya yanalingana na swali lilivyoulizwa na Mheshimiwa Mashimba. Lakini kwa maana ya kutaka afahamu mradi wa kupeleka maji Sumve mpaka Malampaka, tumetenga fedha hizo, mwaka huu, shilingi bilioni mbili, kwanza kwa ajili ya kukamilisha usanifu na makabrasha ya zabuni ili kusudi tuweze kutangaza tender ya kupeleka maji Sumve mpaka Malampaka. Nia ya Serikali ipo palepale, hakuna mabadiliko, hata kama tungesema tu hapa bila utekelezaji ingekuwa haitusaidii, lakini nia ya Serikali ipo na lazima tupeleke maji Sumve, Malya na Malampaka.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kuna utaraibu mzuri wa kuzuia hizo nyavu zisizoruhusiwa, lakini samaki katika maziwa yetu; Ziwa Victoria kuna samaki aina ya sato, nembe, sangara na samaki wengine; lakini kuna utaratibu mzuri katika bahari yetu hasa uvunaji wa samaki aina ya kamba, kwamba wanavunwa baada ya muda fulani halafu wanasimama. Ili samaki hawa waweze kukua katika Ziwa Victoria; sato na samaki wengine; kwa nini sasa tusiwe na utaratibu wa kuzishirikisha nchi za Kenya, Uganda na Tanzania ili kusudi samaki hawa wawe na tija, badala ya kuvua samaki wadogo wadogo tuwe na muda wa kuwavuna? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Ndassa kwa sababu inaelekea ana ufahamu wa ndani kabisa kuhusiana na masuala ya uvuvi. Kimsingi Ziwa Victoria kabla ya miaka ya 1980 samaki aina ya nembe, furu na gogogo walianza kupotea, lakini siku hizi tayari wameshaanza kuonekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la kusimamisha au kusitisha uvuvi katika Ziwa Victoria majadiliano yanaendelea katika ukanda wetu wa Afrika Mashariki kuangalia kama hilo ni suala ambalo linaweza likafanyika. Kwa sababu kimsingi hata sisi Tanzania tukisimamisha leo wenyewe na wengine wakiwa wanaendelea, haitakuwa na faida kwa sababu samaki wale ni migratory. Ukifanya uamuzi katika nchi moja halafu wakaendelea kuvuliwa katika nchi nyingine, bado hautakuwa umepata nafuu yoyote. Kwa hiyo, majadiliano yanaendelea na utafiti vile vile unaendelea. Matokeo yakishatolewa, basi uamuzi sahihi utachukuliwa.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba niiulize Serikali, katika Wilaya ya Kwimba visima 188 vimeharibika, havifanyi kazi kutokana na kuzeeka lakini vingine vimechakaa na vimekauka.
Sasa naomba kuuliza, kwa sababu wananchi wa Kata za Mwabomba na hasa Nkalalo pale center wanashida kubwa sana ya maji kutokana na visima hivi kuharibika, je, Serikali sasa ina mpango gani wa kusaidia ili visima hivyo viweze kufanya kazi wakati tunasubiri mradi mkubwa wa maji ya Ziwa Victoria? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hoja ya Mheshimiwa Ndassa inakwenda katika maeneo mbalimbali na tumekuwa na changamoto kubwa sana katika visima vya maji na ndiyo maana tumekuwa tukitoa maelekezo maeneo mbalimbali kwamba hivi visima vya maji recharging capacity wakati mwingine inashuka kutokana na uharibifu wa mazingira. Hata hivyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Ndassa kwamba katika mpango wa Serikali wa sasa hivi kuna mashindano maalum tumeyatoa kwa kila Halmashauri ya jinsi gani mipango yao mikakati watakavyozindua kuhakikisha miradi ambayo mwanzo ilikuwa haifanyi vizuri wanafanya ukarabati wa visima hivyo na kuweza kuvisimamia. Kuna mpango maalum ambao tumepata fedha kutoka World Bank ambapo zinasaidia sana katika suala zima la kuongeza nguvu za Halmashauri. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba kupitia Halmashauri zetu, ni mpango siyo wa Halmashauri ya Kwimba peke yake isipokuwa ni katika Halmashauri mbalimbali tumewaelekeza wataalam wetu wahakikishe sasa wanavikarabati visima mbalimbali viweze kutoa maji, lakini hata hivyo kuweza kusimamia vizuri kwa sababu baada ya kufanya hivyo watapata fedha nyingine zaidi kwa ajili ya kuhakikisha wanakarabati vituo vyao vya maji. Kwa hiyo, naamini Wilaya ya Kwimba itafanya hili ili wananchi wa maeneo yale waweze kuondokana na shida ya maji katika maeneo yao.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, katika kuitikia wito wa Serikali wananchi wa mikoa ya Mwanza, Simiyu katika majimbo mbalimbali ikiwemo na Jimbo la Bariadi, Misungwi, Sumve pamba imelimwa kwa wingi sana.
Swali langu Mheshimiwa Waziri, endapo wanunuzi wa pamba watashindwa kuinunua pamba yote kwa sababu pamba imelimwa kwa wingi sana msimu huu. Je, Serikali imejipangaje kuwanusuru wakulima hawa ambao wameitikia wito wa Serikali wa kulima Pamba kwa wingi?
MHE. NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali naomba niwaambie wakulima wote wa zao la pamba kwamba tulishakutana na wadau wote wanaolima zao la pamba. Tulishakutana pia na mabenki yote kuhakikisha kwamba pia yale mabenki yanatoa mikopo kwa wafanyabiasha ili waweze pia kutoa mbegu na ukizingatia pia kwamba katika kile Kitalu cha Igunga ambacho kinatoa mbegu bora kabisa ile ya UKM 08 kwamba wakulima wanapata mbegu kwa wingi na vilevile wakulima hao na wafanyabiashara wanapata mikopo kutoka benki ili kuweza kuhakikisha kwamba zao la pamba linazalishwa kwa ufanisi na kwa ubora, ahsante.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, Serikali imesema kwamba itakarabati vituo 205 kikiwemo pia na Kituo cha Afya cha Malya, ninapenda kujua Mheshimiwa Waziri, ni formula gani mnayotumia kupelekwa kwa baadhi ya vituo vya afya shilingi milioni 500 na vingine milioni 400 wakati mlichagua kwamba vituo vyote 205 vikarabatiwe kwa pamoja. Ni formula gani mnayotumia? Lakini ni lini pesa zingine ambazo mliahidi kwamba mtapeleka shilingi milioni 500 kwa kila kituo, kwa nini 400 na kwa nini 500? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni formula gani ambayo inatumika katika kupeleka kupeleka fedha katika vituo vya afya sehemu nyingine milioni 500 sehemu nyingine milioni 400?
Mheshimiwa Naibu Spika, formula zipo nyingi, kwanza ya kwanza inategemea na source of funding, ni nani ambaye ameleta fedha ili ziweze kwenda kwenye kituo cha afya. Lakini pia formula nyingine ni namna ambavyo ukarabati unaohitajika, kuna baadhi ya maeneo ni majengo machache tu ndiyo ambayo yanaongezwa kiasi kwamba ikipelekwa shilingi milioni 400 inatosha kabisa kuweza kufanya ujenzi ule ukakamilika. Kwa hiyo, inategemea source lakini pia na ukarabati ni kwa kiasi gani unakwenda kufanyika katika eneo husika.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana. Maji ni uhai, ningependa kuiuliza Serikali, kwa sababu iko ahadi ya kupeleka maji katika maeneo ya Sumve, Malya, Mwagini kupitia Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria, ningependa Serikali iniambie ni lini hasa mradi huo mkubwa ambao utanufaisha zaidi ya vijiji 40, utaanza kwa sababu ni ahadi ya muda mrefu?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali imeahidi kutoa maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka maeneo ya Sumve na maeneo mengine. Naomba nimhakikishie tu kwamba ahadi hiyo ipo pale pale na nitakapoleta bajeti yangu nitaeleza hilo jibu la lini kazi hiyo itaanza.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na maelezo mazuri sana ya Mheshimiwa Waziri, lakini Serikali imekuwa ikiahidi kwamba itajenga Mahakama za Mwanzo kwa muda mrefu sana. Chikawe one aliahidi, akaja Chikawe two, mama Nagu, Kairuki, ahadi ni ile ile. Sasa ningependa kujua Mahakama ya Nyamikoma, Kata ya Iseni, Jimbo la Sumve Wilaya ya Kwimba itakuwa lini kwenye mpango wa kujengwa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ni kweli, nakubaliana na mawazo ya Mheshimiwa Mbunge kwamba tangu Mheshimiwa mama Nagu, Chikawe na Asha-Rose Migiro tumekuwa tukizungumzia suala la ujenzi wa Mahakama za Mwanzo ikiwemo Mahakama ya Mwanzo ya Sumve.
Mheshimiwa Spika, nioneshe tu katika mwaka wa fedha 2012/2013, Mahakama ilipokea takribani asilimia 51 ya fedha kwa ajili ya maendeleo, mwaka 2013/2014 asilimia 18, mwaka 2014/2015 asilimia 7.5, mwaka 2015/2016 asilimia 100. Kwa hiyo, hoja ninayotaka kuijenga hapa chini ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli tutatekeleza mipango ya maendeleo kama tulivyoainisha katika program ya ujenzi wa Mahakama ikiwemo Mahakama za Mwanzo. Kwa hiyo, hili jambo linawezekana, nataka kumthibitishia Mheshimiwa Ndassa kwamba tutamaliza kuijenga Mahakama ya Mwanzo ya Sumve kama tulivyoahidi kabla ya mwaka wa bajeti wa 2016/2017 haujakamilika.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri, anajua kwamba Mradi Mkubwa wa Maji wa Ziwa Victoria unaanzia katika Kitongoji cha Ihelele, Kijiji cha Nyahumango. Cha kusikitisha Mheshimiwa Waziri, sina tatizo na maji kwenda Nzega, kwenda Kahama au sehemu nyingine, pale kwenye chanzo cha maji Ihelele penye matanki makubwa kuna kituo kimoja tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, hivi ungekuwa wewe ndiyo mwenye Jimbo hilo na una Waziri ungejisikiaje?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ningekuwa sijafanya ziara ningeshtuka sana, lakini kwa sababu sijawahi kwenda kwenye eneo hilo nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba nitaenda nikaone kwa nini vijiji ambavyo vinazungukwa na matenki makubwa ya maji havipati maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa ziara yangu Mkoa wa Mtwara, nilikwenda eneo la Mbwinji. Eneo la Mbwinji lina matanki makubwa sana ya maji ndiyo chanzo cha maji, kitu cha ajabu nilikuta wananchi wanaokaa lile eneo hawapati maji. Nilivyojaribu kuuliza ikaonekana kwamba maji pale yakishachotwa lazima yapelekwe Masasi kwenda kufanyiwa sasa utibabu, kuwekewa dawa ili yaweze kuwa safi kwa ajili ya matumizi ya binadamu, ndiyo baadaye sasa yaweze kusambazwa kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilipofika pale niliagiza na sasa hivi wananchi wa maeneo yale tayari wanapata maji. Sasa sielewi hilo eneo analozungumza Mheshimiwa Mbunge, linaweza likawa na tabia ya kufanana na hiyo kwamba, hapo ndipo wanapochota maji, wanaweka kwenye matenki halafu baadaye yanakwenda kwenye mtambo wa kutibu maji. Sasa, japo sijafika lakini naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hili suala nitalifuatilia na nitamjibu kabla hatujamaliza Bunge hili.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Tanzania tunayo makampuni binafsi mawili yanayotoa huduma za ndege kwa wasafiri hapa nchini, FastJet pamoja na Precision.
Mheshimiwa Spika, lakini ningependa kujua ni utaratibu gani wa gharama za nauli wanazotumia kupanga. Kwa sababu gharama ya kutoka Dar es Salaam kwenda Mwanza na kurudi inakaribia shilingi 800,000 vivyo hivyo gharama ya kutoka Dar es Salaam kwenda Mbeya inakaribia shilingi 800,000 sawasawa na nauli ya kutoka Dar es Salaam kwenda Dubai kwa ndege za Emirates. Nataka kujua, ni utaratibu gani unaotumika kupanga gharama za nauli kwa wasafiri hasa kwa Dar es Salaam, Mwanza pamoja na Mbeya, routes za ndani hizi ni nani anayepanga nauli hizi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, nauli za ndege kwa sasa zinapangwa na soko.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, kinachotokea taasisi yetu ya SUMATRA huwa inafanya kazi ya kuangalia kama hizo nauli ambazo hupangwa na soko na pengine soko haliko sawasawa inafanya utaratibu wa kurekebisha.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, kikubwa ambacho Serikali imeamua ni kufufua Shirika letu la ATCL liwe na ndege za kutosha ili tuweze kuondoa ukiritimba wa kampuni chache zinazotoa huduma za ndege kwa sasa, hatimaye bei ya soko iwe kweli bei ya soko. (Makofi)


SPIKA: Majibu ya nyongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Mbarawa.
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri zinapangwa na soko lakini Mamlaka ya TCA (Tanzania Civil Aviation) ndiyo inasimamia jambo hili. Kwa kulijua hili, Serikali inafanya kila linalowezekana tuweze kufufua Shirika la Air Tanzania na ambapo sasa tuna utaratibu wa kununua ndege mbili, Q400, wakati wowote zitaweza kufika hapa Tanzania kuhakikisha kwamba bei hiyo sasa tunaisimamia ipasavyo.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu TBC 1 na TBC Redio ni visemeo vya Taifa, ndiyo spika ya Serikali. Je, kwa sababu matatizo ni mengi, usikivu karibu nchi nzima hawasikii vizuri, Je, Mheshimiwa Waziri hivi unatambua kwamba TBC1 na Redio TBC 1, televisheni ni kisemeo cha Taifa. Kwa nini sasa Serikali isiwekeze ili kuondoa kutokusikia vizuri katika maeneo mbalimbali?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Seneta Ndassa kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa TBC katika nchi hii na ndiyo maana umeona uwekezaji ukiongezeka kila mwaka. Sasa hivi tupo katika kuboresha usikivu katika Wilaya tano kwa pesa tuliyoongezewa tuna uwezo kuongeza usikivu katika Wilaya zingine 15. Kwa hiyo, tunapoongeza hizo Wilaya 15 tunaenda kuangalia sehemu ipi ambayo ina hali mbaya zaidi tutaendelea kuboresha hii bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na matatizo ya kifedha, sasa hivi tumeanza kuangalia pia mifumo yetu ya ndani ambayo imekuwa ikitunyima kupata kipato zaidi. Tuna mikataba ambayo mmekuwa mkiipigia kelele hapa kama StarTimes, tumeanza kuchunguza, ninakuhakikishia kwamba katika zoezi tunalolifanya sasa hivi kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais tutafika mahali pazuri. Kwa taarifa tu kwa Bunge hili lako Tukufu Mheshimiwa Rais wa StarTimes Group kutoka China imebidi naye afunge safari kama mwenzetu wa makinikia kuja kutuona kwa ajili ya suala hilo.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nilikuwa naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, barabara ya Isandula iliyoko Magu kwenda Jojilo mpaka Hungumalwa iko kwenye mpango wa kujengwa kwa lami na usanifu ulishafanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ziko barabara mbili, barabara ya Kamanga kwenda Sengerema kwa Mheshimiwa Ngeleja, Mkoani Mwanza; tungependa kujua barabara hizi ambazo ni ahadi ya muda mrefu, ni lini hasa ujenzi wa lami katika barabara hizo utafanyika? Ningependa Mheshimiwa Waziri anipe majibu kwa sababu tumekuwa tukiuliza barabara hizi mara nyingi humu Bungeni, ni lini, ni lini barabara hizi zitajengwa kwa kiwango cha lami?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima niliyonayo kwa Mheshimiwa Ndassa sikutarajia aulize swali, hasa maswali haya ambayo amekuwa akiyarudia na muda wote nimekuwa nikimwambia kwamba mzee wangu ambaye umekaa humu kwa muda mrefu, usihangaike kuendelea kuuliza maswali haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hii iko makini, na nikuhakikishie tumeanza mipango na wataalam wamesikia uliyouliza hapa, kama ambavyo walisikia kule nyuma ulipouliza, wanaendelea kulifanyia kazi, na tutakapopata jibu sahihi tutakuletea. Kikubwa tunachokuahidi ni kwamba barabara hizi ni ahadi za viongozi wetu, na ni lazima ahadi hizi zikamilike kama zilivyo ahadi zingine zote za barabara sehemu mbalimbali za nchi. (Makofi)
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Bwana Waziri naomba nikuulize swali. Serikali ina mpango gani mahususi kwa ajili ya kutumia mabonde yetu kama Ziwa Nyasa, Ziwa Tanganyika, Ziwa Victoria pamja na Mito mikubwa, Serikali ina mpango gani mahususi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tuna mabonde tisa katika Nchi yetu na mpango mahususi tayari tunaanzisha commission kwa kila bonde kwasababu mabonde mengine ni kwamba matumizi ya maji yako shared na nchi zingine kwahiyo kupitia kwenye hizo commission ndiyo tunaratibu maji tuyatumiaje, tutatumia kwa maji safi na salama kama tunavyoyatoa Lake Victoria kupeleka Igunga lakini pia tutatumia kwa ajili ya vilimo vya umwagiliaji. Kwa hiyo, tunao mpango mahususi kuhakikisha kwamba mabonde yote tuliyonayo ambayo yako nchini kwetu tunayatumia vizuri kwa ajili ya umwagiliaji na pia kwa ajili ya maji safi na salama na maana ya mabonde ni nini? Ni pamoja na maziwa na mito.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu TBC 1 na TBC Redio ni visemeo vya Taifa, ndiyo spika ya Serikali. Je, kwa sababu matatizo ni mengi, usikivu karibu nchi nzima hawasikii vizuri, Je, Mheshimiwa Waziri hivi unatambua kwamba TBC1 na Redio TBC 1, televisheni ni kisemeo cha Taifa. Kwa nini sasa Serikali isiwekeze ili kuondoa kutokusikia vizuri katika maeneo mbalimbali?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Seneta Ndassa kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa TBC katika nchi hii na ndiyo maana umeona uwekezaji ukiongezeka kila mwaka. Sasa hivi tupo katika kuboresha usikivu katika Wilaya tano kwa pesa tuliyoongezewa tuna uwezo kuongeza usikivu katika Wilaya zingine 15. Kwa hiyo, tunapoongeza hizo Wilaya 15 tunaenda kuangalia sehemu ipi ambayo ina hali mbaya zaidi tutaendelea kuboresha hii bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na matatizo ya kifedha, sasa hivi tumeanza kuangalia pia mifumo yetu ya ndani ambayo imekuwa ikitunyima kupata kipato zaidi. Tuna mikataba ambayo mmekuwa mkiipigia kelele hapa kama StarTimes, tumeanza kuchunguza, ninakuhakikishia kwamba katika zoezi tunalolifanya sasa hivi kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais tutafika mahali pazuri. Kwa taarifa tu kwa Bunge hili lako Tukufu Mheshimiwa Rais wa StarTimes Group kutoka China imebidi naye afunge safari kama mwenzetu wa makinikia kuja kutuona kwa ajili ya suala hilo.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri kwamba barabara ya kutoka Magu (Ilungu) – Nkalalo – Ngudu - Hungumalwa ni barabara muhimu sana katika kuleta uchumi kwa maeneo yale na imeshafanyiwa usanifu wa kujengwa kwa kiwango cha lami. Je, ni lini sasa barabara hiyo itajengwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwani amekuwepo katika Bunge hili muda mrefu na naamini kabisa hata hii hatua ya barabara hii kusanifiwa na kupata michoro ni pamoja na juhudi zake mwenyewe. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Ndassa tuendelee kuwasiliana kuifuatilia barabara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme kwamba Serikali ilikuwa inafanya juhudi kubwa sana za kuunganisha mikoa. Baada ya kuwa sasa tumekuwa na hatua nzuri, naamini tutaendelea kutafuta fedha na muda siyo mrefu barabara hii ya Ilungu – Ngudu – Hungumalwa tutaweza kuitafutia fedha ili tuweze kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimuombe tu uvute subira yeye na wananchi wake muda siyo mrefu tutaipatia ufumbuzi barabara hii.
MHE. RICHARD M. NDASA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Magonjwa yako mengi kama alivyosema huu ugonjwa wa Lupa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ugonjwa wa Ebola ni hatari sana. Ugonjwa huu umejitokeza nchini DRC Congo (Kivu Kaskazini) na umeshaua zaidi ya watu 77 na watu 116 wamegundulika wana ugonjwa huu na kwa sababu sisi Congo, Kivu Kaskazini inapakana na Rwanda, Burundi na Uganda: Je, Serikali kwa sababu ugonjwa huu ni hatari sana, tunamwomba Mwenyezi Mungu apishie mbali ugonjwa huu usije kwetu nchini; Serikali imejipangaje kukabiliana na ugonjwa huu hatari na mbaya sana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Ebola ni ugonjwa hatari na unaambukiza kwa haraka sana na mara nyingi ugonjwa huu hauna tiba na wale wanaopata ugonjwa huu zaidi ya asilimia 50 hawaponi, huishia kufariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwa takwimu ambazo amezitoa Mheshimiwa Mbunge kwamba wenzetu katika nchi ya DRC limejitokeza balaa hili la ugonjwa wa Ebola na mpaka sasa hivi zaidi ya watu 76 wamefariki na zaidi ya 100 wameugua ugonjwa huu. Sisi kama Tanzania tumechukua hatua gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tumeimarisha mifumo yetu ya ufuatiliaji wa wagonjwa katika mipaka yetu yote kwa kuhakikisha kwamba watu wote wanaoingia nchini katika maeneo ambayo tunayahisi yanaweza yakawa ugonjwa huu, tumeimarisha mfumo wa ufuatiliaji; tumeweka thermo scanner, tumeweka maeneo mahususi kwa wale watakaoingia nchini ambao tunawahisi wana dalili, tunawatenga, tumeweka hizo isolation center.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumetoa elimu ya kutosha katika mikoa yetu ambayo ipo mipakani kwa viongozi wote wa Serikali pamoja na watoa huduma wetu wa afya ili endapo mgonjwa ataingia nchini, waweze kuchukua hatua kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesambaza vifaa vya kujikinga (personal protection equipment) katika maeneo yote ambayo yapo pembezoni ili watoa huduma wetu na wale ambao wataingia, watakutana na wale wagonjwa waweze kujikinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeimarisha mifumo yetu ya maabara, endapo tutapata mgonjwa ambaye atahitaji kuchukuliwa sampuli, tumenunua vifaa, tunavyo na maabara tumeziandaa.
Mwisho kabisa, tumeendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusiana na gonjwa hili kuu, kwamba endapo mtu atamwona mtu ambaye ametoka katika nchi za jirani ana dalili za homa, ana maumivu ya viungo ama kutoka damu sehemu mbalimbali za mwili, wananchi waweze kutoa taarifa kwa haraka katika mamlaka na kuchukua tahadhari ya kutomshika mtu yule ambaye ana dalili zile ambazo nimezigusia. (Makofi)
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naomba nimuulize bwana Waziri.
Mheshimiwa Bwana Waziri TASAF One ilifanya vizuri sana, TASAF Two nayo imefanya vizuri, na pia sasa TASAF Three nayo inaendelea vizuri. Lakini Mheshimiwa Waziri vipo viporo vya TASAF Two mfano, Barabara ya Bungulwa kwenda Hundya ambayo ilitengeneza makalavati 100, yapo pale Bungulwa zaidi ya miaka mitano sasa. Barabara ya Chibuji - Upamwa miaka mitano zaidi ilikuwa ilete pesa za ukamilishaji wa miradi hiyo miwili ya barabara ni viporo.
Mheshimiwa Waziri Mkuchika ni lini viporo hivyo vya barabara hizo vitaletwa ili kusudi barabara zitengenezwe?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la rafiki yangu Mheshimiwa Ndasa kama ifuatavyo kuhusu viporo anavyouliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuagiza Mkurugenzi wa TASAF huko aliko anakonisikiliza apeleke timu katika maeneo hayo, nipate taarifa ya hiyo miradi na baadae nitafanya maamuzi.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri kwamba, barabara ya kutoka Isandula, Magu inayopita Bukwimba kuja Ngudu mpaka Gungumalwa ni ahadi ya siku nyingi kwamba itatengenezwa kwa kiwango cha lami. Tungependa kujua sasa kwa sababu mwanzo tuliambiwa kwamba upembuzi yakinifu umeshakamilika, upembuzi wa kina umeshakamilika, wananchi wa Magu, Kwimba wanataka kujua sasa barabara hiyo itaanza kujengwa lini kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa sababu mara nyingi sana amekuwa akifuatilia barabara hii. Niseme tu kwa ufupi kabisa upembuzi wa kina unaendelea kukamilishwa, ni hivi tu jana Meneja wa TANROAD, Mkoa wa Mwanza amepokea report ya awali ya usanifu wa kina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo tunafanya mapitio ili sasa tuweze kukamilisha zoezi hili. Zoezi hili likikamilika litatuwezesha kujua gharama za mradi ili sasa tuiweke kwenye bajeti na hatimaye tutafute fedha kwa ajili ya kuijenga barabara hii kutoka Isandula Magu kupitia Bukwimba kuja Hungumwalo.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Tarehe 11 Julai, 2017, narudia tarehe 13 Julai, 2017 Mheshimiwa Waziri alikuja Nyamatala kuzindua umeme Kimkoa na uzinduzi ulifanyika katika Kijiji cha Nyamatala hadi leo ni kijiji kimoja tu ambacho kimeshawashwa umeme lakini kisingizio wanasema hakuna nyaya, nguzo na transfoma. Naomba majibu ya Serikali, hivi vijiji ambavyo vilikuwa vimepangwa kuwashwa umeme vitawashwa lini?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Ndassa na kwa kweli niseme tu katika Mkoa mzima wa Mwanza nitoe marekebisho kidogo ya hoja ya Mheshimiwa Ndasa, ni vijiji 21 tayari vimeshawashwa umeme siyo kijiji kimoja. Ni kweli kabisa katika jimbo lake Kijiji cha Nyamatala ambapo tulifanya uzinduzi tayari kimeshawashwa umeme na sasa wanaendelea na kijiji kinachofanya kwenda Sangabuye. Nikubaliane na Mheshimiwa Ndassa kwamba speed ya mkandarasi haikuwa nzuri, lakini tangu wiki iliyopita ameshaleta nguzo 500 katika jimbo lake ni matarajio yetu kwamba sasa speed itaongezeka. Nimwombe Mheshimiwa Ndassa tushikiriane atuletee maeneo yenye changamoto ili kazi iianze kutekelezwa haraka iwezekanavyo.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nimuulize swali Mheshimiwa Waziri; barabara ya kutoka Mwanza kwenda Shinyanga Boarder yenye urefu wa kilometa 102 iliyojengwa mwaka 1994 -1998 ni mbaya sana kwa sasa, ina zaidi ya mashimo 3,032 na imekuwa ikifanyiwa utengenezwaji wa mara kwa mara. Je, Serikali inaweza sasa kusema ni lini barabara hii itajengwa upya?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakiri Serikali tunafahamu ubovu wa barabara aliyoitaja Mheshimiwa na kwa kweli ina mashimo mengi na ni kero sana kwa wapitaji na watumiaji wa barabara ile. Nimhakikishie Mheshimiwa Ndassa kwamba Serikali iko kwenye mpango wa kufanya ukarabati mkubwa kwenye barabara ile na hali ya kifedha itakapoimarika Mheshimiwa Ndassa atatuona tukiwa maeneo yale na wataalam kwa ajili ya kurekebisha kipande hicho cha barabara.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri; kwa sababu Jimbo la Sumve lina visima 89 ambavyo ni vibovu havitoi maji, na barua unayo; je, ni lini visima hivyo sasa vitatengenezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti,...
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua changamoto hizo na viporo mbalimbali Waziri wangu akaona haja sasa kwa Wabunge wote kupitisha barua kuangalia namna gani na kuorodhesha maeneo ambayo yenye changamoto. Labla nimuombe Mheshimiwa Mbunge jambo hili baada ya kulichukua tutalifanyia kazi kwa wakati na yeye katika maeneo yake hatomuacha katika kuhakikisha tunamrekebishia visima vyake, ahsante sana.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Jimbo la Sumve lina shule za sekondari 17 ikiwemo Shule ya Sekondari ya Talo ambayo inazo sifa zote kama vile miundombinu na tumeshaleta maombi Serikalini. Je, ni lini sasa shule hiyo ya sekondari itawekewa kidato cha tano na sita?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ndassa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimeendelea kusema kwenye majibu yaliyopita, Wizara ya Elimu ipo tayari kupokea maombi ya kutoka kwenye halmashauri zinazofikiri zinataka shule ziweze kupatiwa ruhusa ya kuendesha kidato cha tano na sita. Sisi tutakachofanya tutaenda kujiridhisha na hali ya miundombinu kuangalia kama kweli kuna mazingira ya kukidhi kuanzishwa kidato cha tano na sita. Kama nilivyosema, lengo letu kama Wizara tunataka angalao tuhakikishe kwamba katika kila tarafa kuwe na kidato cha tano na sita. Kwa hiyo, tukiangalia mazingira kama yanaridhisha sisi hatuna shida. Kwa hiyo, naomba waanze wao walete mapendekezo Wizarani na sisi tutayafanyia kazi.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mheshimiwa Waziri, kama Waziri mwenye dhamana, nyumba za Magereza zilizoko pale Isanga hazifai, hazifai, hazifai kabisa kukaliwa na binadamu.
Mheshimiwa Spika, hata wewe kwa sababu ni mtu wa Dodoma, ukienda pale ukiona zile nyumba utasema hizi nyumba wanakaa binadamu? Naomba kupata tamko la Serikali, lini nyumba hizo zitajengwa upya kwa ajili ya Askari wetu hawa wa magereza katika Gereza Kuu la Isanga?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Spika, ni kweli hata katika Jeshi la Magereza tuna changamoto ya uhaba wa nyumba na uchakavu wa nyumba za Askari Magereza. Ndiyo maana tunatumia njia mbalimbali ukiachilia mbali utaratibu wa kawaida wa kibajeti, tumekuwa tukitumia rasilimali katika maeneo husika kuzikarabati nyumba hizo, hasa ukitilia maanani kwamba,
Jeshi la Magereza lina kitengo madhubuti kabisa kinachojishughulisha na ujenzi pamoja na nguvu kazi ya wafungwa.
Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukifanya hivyo maeneo mbalimbali katika nchi, lakini fursa kubwa ambayo inaangukia katika Gereza la Isanga lililopo Dodoma ni juu ya hatua ya Serikali kuhamisha Makao Makuu yake rasmi kuja Dodoma. Jambo hilo limesababisha sasa hivi kuwa na fursa pana ya kutanua wigo wa mazingira ya ufanyaji kazi pamoja na makazi ya Askari wa vyombo vyetu vyote. Ndiyo maana mtaona sasa hivi kwamba, katika eneo la Magereza, Uhamiaji na Jeshi la Polisi kuna maendeleo makubwa ya kuboresha makazi ya Askari Dodoma ili kwenda sambamba na kasi ya ongezeko la ukuaji wa Mji wa Dodoma kutokana na maamuzi thabiti ya Serikali ya kuhamishia Makao Makuu Dodoma.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, Nimemsikiliza vizuri Mheshimiwa Naibu wakati akijibu swali nilikuwa nataka nimuulize tu ikitokea mwanafunzi wa kiume akamchukua Mwalimu wa kike sheria inasemaje?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Elimu ya Mwaka 1978 na kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2002, Sura ya 353 imezungumza katika kifungu cha 60A(2) kwamba ni kosa pia kwa mtoto wa kiume yeyote ambaye yuko shule kuoa. Kwa hiyo, kosa linabaki pale pale na kwa upande wa wanaume imezungumza kama ni kosa, kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge Mheshimiwa Ndassa bado inabaki pale pale mtoto wa kiume pia na yeye akioa akiwa bado yuko shuleni ni kosa pia.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, tarehe 13 Julai, 2017 aliyekuwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini ambaye sasa ni Waziri wa Nishati alikuja kuzindua Mradi wa REA III katika Kijiji cha Nyamatala, Kata ya Ngula lakini hadi leo ni miezi saba hakuna hata eneo moja umeme umeshawaka. Nataka nipate majibu ya Serikali miezi saba sio Kitongoji, Kijiji wala Kata na uzinduzi huo ulikuwa kimkoa. Nataka nipate majibu ya Serikali tatizo hasa ni nini na umeme huu utaanza kuwaka lini.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba ni kweli katika Mkoa wa Mwanza mkandarasi wa Nippo Group Limited yupo kazini na ninaomba nimfahamishe baada ya uzinduzi ule kazi ambazo ziliendelea ni pamoja na tathmini, uchambuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niliarifu Bunge lako kipindi kile ambapo miradi inazinduliwa yapo mahitaji mbalimbali ambapo yalijitokeza kutoka kwa Wabunge kutokana na uhitaji wa nishati hii Vijijini. Kwa hiyo, tathmini ya ilivyokuwa inaendelea kufanyika na maeneo mbalimbali ambako wakandarasi walikuwepo, vipo Vijiji pia vya nyongeza pia vimeongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtaarifu kwamba kwa Mkoa wa Mwanza mpaka sasa mkandarasi yule ameshawasha Vijiji sita lakini naomba nimwelekeze Mkandarasi Nippo tulitoa maelekezo kwa wakandarasi wote wafanye kazi katika Wilaya zote, wawe na magenge ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pengine changamoto inayojitokeza mkandarasi huyu yupo katika Wilaya zingine hajafikiwa katika Jimbo lake. Lakini naomba nimthibitishie na wizara kwa awamu hii imepanga kufanya ziara katika Jimbo lake na kazi zitaendelea na kwa sababu mikataba hii inaonyesha na muda wa kazi ni kuanzia kipindi hiki mpaka Novemba, 2019 ndio zinakamilika, naomba nimtoe wasiwasi yeye Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Jimbo lake kwamba huduma hii ya umeme vijijini kama ilivyozinduliwa itapatikana kwasababu mkandarasi yupo ndani ya wakati, asante sana.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri katika swali la Mheshimiwa Ndassa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Ndassa kwa kweli wakati tunakwenda kuzindua alifanya kazi kubwa sana, lakini nimpe taarifa katika Jimbo lake tayari wakandarasi wapo katika Kijiji cha Nyamatara na Nyambiti; na Nyambiti na Nyamatara kesho wanawasha umeme. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge awasiliane na Mheshimiwa Katibu wake na jana tuliwasiliana naye pale Nyamatara wameshasimika nguzo, transfoma wamepeleka juzi na kesho na keshokutwa wataendelea kuwasha kwenye vijiji viwili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vya Nguge pamoja na Nipo katika Mkoa wa Mwanza pia wameshawasha umeme lakini pamoja nahayo nitawasiliana na Mheshimiwa Ndassa tukae naye vizuri ili maeneo mengine vipaumbele tuweze kuwapelekea umeme haraka iwezekanavyo.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nilikuwa naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri, je, anajua kwamba mpaka sasa Bodi ya Pamba haijatoa leseni kwa wanunuzi wa pamba na sababu ni nini?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumjibu Mheshimiwa Ndassa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo swali lake moja dogo la nyongeza kuhusu Bodi ya Pamba kutotoa leseni mpaka sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba sasa hivi tuko kwenye mchakato wa kuhakikisha kwamba Bodi ya Pamba inatolewa leseni na haitazidi mwezi ujao leseni itakuwa imetolewa. Ahsante.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na maelezo mazuri sana ya Serikali, barabara hii imekuwa na maelezo ya muda mrefu kwa maana ya kwamba kuna ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne na Rais wa Awamu ya Tano kwamba barabara hiyo itatengenezwa kwa kiwango cha lami. Kwa maelezo ya Mheshimiwa Waziri anasema kwamba usanifu wa kina utakamilika Mei, 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Barabara Mkoa wa Mwanza. Usanifu wa kina umeshakamilika na baada ya usanifu wa kina kukamilika nilienda kwa Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, ofisini kwake, akaniahidi kwamba ataiingiza kwenye bajeti ya mwaka huu kwa maana ya 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka kuuliza, kwa maelezo haya, Barabara ya Isandula – Hungumalwa itaingizwa kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha 2019/2020?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kama ahadi inatolewa na Mheshimiwa Rais na Serikali imekiri kwamba barabara hii ni muhimu na ni kiungo kikubwa kwa Sirari, Mwanza na Shinyanga: Je, Serikali sasa kwa umuhimu huo, iko tayari barabara hii ambayo ni muhimu kuiingiza kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza unipe ruhusa nimpongeze sana Mheshimiwa Richard Ndassa, Senator huyu, amekuwa akiifuatilia sana barabara hii na ni kweli barabara hii imeahidiwa muda mrefu na ni kweli kabisa Mheshimiwa Mbunge amekuwa akiifuatilia sana barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa umuhimu huo, tumesimamia vizuri kuhakikisha kwamba usanifu unakamilika. Tulipokea rasimu ya kwanza ya usanifu wa barabara hii ambayo angalau ime-indicate kwamba barabara hii inaweza ikawa na gharama gani. Kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa Ndassa avute subira na kwa sababu jambo hili tumelishika na tumedhamiria kujenga barabara hii na sisi tunaitazama barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili amezungumza juu ya bajeti, niseme tu kwamba asiwahishe shughuli, tunaitazama vizuri barabara hii, na Mungu akijaalia tunaweza tukaja na mapendekezo ya kuijenga barabara hii. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Ndassa pamoja na wananchi wa Isandula, Bukwimba, Nyambiti, Ngudu, Nyamilama, Hungumalwa (Magu), Sumve na Ngudu kwa ujumla kwamba tunaona umuhimu wa kuijenga barabara hii. Tukipata fedha na bajeti ikiruhusu tutaijenga barabara hii kwa kiwango cha lami.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Tulipitisha azimio humu Bungeni kwamba msimu wa pamba unatakiwa uanze tarehe Mosi Mwezi Mei kila mwaka. Hivi sasa kuna Walanguzi tayari wameshaanza kupitapita na kununua Pamba kwa shilingi mia tano, mia sita, mia saba. Je, ni nini tamko la Serikali?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali la Mheshimiwa Ndassa (Senator) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Mheshimiwa Senator ni taarifa muhimu sana kwa Wizara ya Kilimo kwa sababu tarehe 29 Aprili, tulifanya Mkutano wa 15 wa wadau wa pamba na baada ya hapo jana tulikuwa tuna kikao cha kupitia mwongozo wa msimu wa ununuzi wa pamba na leo hii tunapitia masuala ya bei elekezi ili kuanza msimu tarehe Mosi Mei, 2019 na taratibu hizi zote ziko kisheria, kwa hiyo yoyote yule ambaye ananunua pamba kabla ya uzinduzi wa msimu wa pamba ambao uko kisheria ni ukiukwaji wa sharia. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Ndassa baada ya hapa nitawasiliana na Wakuu wa Mikoa na kuhakikisha Serikali tunajipanga kuhakikisha mkulima hanyonywi…

MWENYEKITI: Ahsante, ameshakuelewa.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA): …kwa sababu shilingi mia sita au mia saba ni hela ndogo sana kwa mkulima.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba nimuulize swali Mheshimiwa Waziri katika Mkoa wa Mwanza, katika mgao wa fedha za maboma kwa ajili ya sekondari, Wilaya ya Kwimba haikupangiwa hata senti tano kwa maana hata boma moja, ilisahaulika na tayari tulikuwa tumeshaleta Shule za Sekondari za Wala, Kikubiji, Malya, Wungumarwa, Ndami, Mwabomba, Shilembo, Iseni na Mwangalanga. Mheshimiwa Waziri, tunaomba tupate majibu kwa nini Wilaya ya Kwimba katika mgao huo wa bilioni
29.9 ilirukwa yenye Majimbo mawili na tayari tulikuwa tumeshaweka majina.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mheshimiwa Mbunge ameshawasilisha hoja yake hiyo Wizarani na nilimuahidi kwa niaba ya Wizara kwamba watakapoanza kugawa fedha za EPFR sekondari maeneo yote siyo kwake tu, maeneo yote ambayo yalivukwa kwa bahati mbaya maana huo haukuwa mpango mahsusi wa makusudi, ilikuwa ni bahati mbaya tu, tutazingatia Kwimba pamoja na maeneo mengine yote ambayo yalirukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, niombe, wakati tunaomba taarifa hizi, ndiyo maana nikasema hapa Wakurugenzi na maafisa elimu wetu wa sekondari na msingi, wanapoombwa walete taarifa ya maboma TAMISEMI tunawaelekeza washauriane na kupeana taarifa na Wabunge ili wazungumze kwenye lugha moja. Imegundulika kuna maboma mengine yameletwa na Waheshimiwa Wabunge lakini kule wanasema kwamba hiyo siyo shida kubwa sana. Kwa hiyo, tumesema tunaposema tunahitaji maboma, wakurugenzi na maafisa elimu wakitoa taarifa wapitishe au kushauriana na Waheshimiwa Wabunge ili tuzungumze pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo, fedha zikipelekwa kama zilivyopelekwa sasa, tumepeleka bilioni 29.9 kuna baadhi ya Wabunge hawakupewa taarifa, tumepeleka bilioni 68.48 wiki iliyopita, inawezekana Wabunge hawajui;
kwa hiyo, Wabunge wajulishwe ili wajue lakini kama kuna mahali pesa imeletwa kwenye halmashauri una hali mbaya sana kwenye shule ya msingi au sekondari, mkurugenzi anajua anaandika barua kwa Katibu Mkuu TAMISEMI anaomba kubadilisha matumizi ili kutibu shida kubwa, hii nyingine itaendelea kusubiri, asante.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba niishukuru sana Serikali kwa majibu yake mazuri hasa kukamilisha angalau kupeleka maji katika Wilaya ya Magu pale Magu Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu; kwa sababu muuliza swali la msingi amezungumzia vijiji kadhaa ikiwemo pamoja na Kijiji cha Kabila ambacho kina wakazi wengi sana. Ili kuondoa tatizo la ukosefu wa maji na Mheshimiwa Waziri anajua kabisa kwamba maji ni uhai, ni lini sasa angalau kwa kuanzia kabla ya Mradi mkubwa huu wa Maji ya Ziwa Victoria haujaanza angalau kwenda kufufua vile visima ambavyo vilikuwepo kama ambavyo tunavyofanya sasa kwenye eneo la Jimbo la Sumve pamoja na Magu, lakini pia kusafisha vile visima ambavyo vilikuwa vinafanya kazi. Sasa Serikali kwa nini sasa isifanye utaratibu wa kuchimba na kusafisha vile visima ambavyo vilikuwepo? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndassa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mzee wangu, Mzee Ndassa sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji tumeainisha Mikoa zaidi ya 17 yenye changamoto ya maji ikiwemo eneo la Mkoa wa Mwanza, lakini tumepata fedha kutokea World Bank na katika Mikoa hii 17 tumepeleka kila Halmashauri 1.3 billion ikiwemo katika Jimbo lake la Sumve.

Nimwombe sana Mhandisi wa maji akae na Mheshimiwa Mbunge na mimi mwenyewe nipo tayari ili katika kuhakikisha fedha zile zinaelekezwa katika zile changamoto ambazo Mheshimiwa Mbunge amezianisha. Ahsante sana.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la msingi lilikuwa linazungumzia ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami. Mheshimiwa Waziri ningependa kujua sasa kwa sababu tunayo barabara yetu ya kutoka Isandula inayopita Mkalama na kwenda Ngudu mpaka Hungumalo. Ningependa kujua sasa ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami ili kuchachua maendeleo na uchumi katika Mji wa Ngudu.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara yangu imeshakamilisha usanifu wa awali na upembuzi yakinifu wa barabara hii muhimu ambayo Mheshimiwa Mbunge anaitaja. Barabara hii inapita kwenye Majimbo matatu kama alivyozungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuhakikishie Mheshimiwa Ndassa baada ya kukamilisha zoezi hili ambalo barabara hii ina urefu wa kama kilometa 60 hivi na kidogo ambayo inaanzia kule Isandula, inakuja Ngudu, Nyaminama inapita Mabuki hadi kule Hungumalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa vile tumeshamaliza zoezi la usanifu na kutambua gharama za barabara hii, tunajipanga tukipata fedha nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa eneo lako hili kwamba tutaanza ujenzi wa barabara ya lami. Tunajua inapita katika maeneo ambayo ina uchumi mkubwa, ahsante sana.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba uniruhuru niipongeze sana Serikali kwa hatua ambayo sasa imefikia kwa sababu kilio kikubwa kwa wakulima wapamba ni kwamba pamba hiyo inatakiwa iongezewe thamani.

Sasa swali langu nimesema kwamba upembuzi tayari umeshakamilisha na viongozi wakuu wa mifuko hii wako Mwanza nasikia, sasa ni lini sasa baada ya hiyo Februari kwa sababu majibu haya yanaweza kusema kwamba ni Februari kumbe ni mwezi mwingine, ni lini sasa hasa ujenzi wa vinu hivi vitatu kwa maana ya hii Nyambiti Ginnery, Ngasamo Ginnery pamoja Kasamwa Ginnery.

Lini vitaanza kujengwa ili zao la pamba lipate thamani zaidi? Nakushuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTHONY P. MAVUNDE): Mheshimiwa Spika, niruhusu kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo anawapigania wakulima wa pamba wa Kanda ya Ziwa na amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba zao hili linaongezwa thamani. Kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema leo wakurugenzi wote wa uwekezaji wa mifuko hii wako Mwanza na kesho kuna kikao cha Wakurugenzi Wakuu ambao kupitia kikao hicho tutapata way forward ya lini taratibu hizi zitaanza kwa sababu kesho wanakutaka kwa ajili ya mambo ya kitaalam, hivyo nimuombe Mheshimiwa Ndasa awe mvumilivu tusubiri taarifa ya Wakurugenzi Wakuu kesho ili tujue way forward ni nini. Nashukuru.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana. Nimemsikiliza vizuri sana Mheshimiwa Naibu Waziri. Swali langu ni dogo sana, kwa sababu sasa wakulima wa pamba tayari wameshalima pamba yao lakini tatizo lililopo hivi sasa hakuna viuadudu ambavyo vimeshapelekwa. Bwana Waziri wewe, najua wewe ni champion wa pamba, ni lini dawa za kuua wadudu zitapekwa kwa wakulima wetu wa zao la pamba?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Spika, nataka nimjibu Mheshimiwa Senata Ndassa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hivi sasa tunavyoongea usambazaji wa viuadudu umeanza katika maeneo ambayo wakulima walianza kulima mapema mwezi Oktoba, katika baadhi ya Wilaya za Mkoa wa Geita. Mpaka sasa tumeshasambaza chupa laki tisa na zoezi la usambazaji linaendelea.

Mheshimiwa Spika, lakini kutokana na kalenda tutahakikisha viuadudu vinafika kwa wakati. Kwa mujibu wa kalenda wakulima wanatakiwa kupulizia mara ya pili kuanzia tarehe 15 Februari, tunahakikisha kwamba wakulima wote watapata dawa kwa wakati. Ndani ya Serikali na Bodi ya Pamba mchakato unaendelea na taasisi za fedha zimeshajitokeza kuhakikisha kwamba dawa zinapatikana.

Mheshimiwa Spika, nitumie Bunge hili kuomba, kilimo cha pamba kwa miaka yote kimeendelea kutegemea mgogo wa Serikali. Pamba ni zao ambalo limelimwa kwa muda mrefu likitegemea kubebwa na Serikali. Niombe na nitumie nafasi hii umewadia wakati wa zao la pamba kusimama lenyewe, dawa ziuzwe katika maduka kama wakulima wengine wanavyopata, mbegu zipatikane na sisi kama Serikali tunajenga huo mfumo ili bidhaa hizi zisiwe tena mpaka zitengemee intervention ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, tumekubaliana hakuna dawa wala mbegu ya bure. Nitumie Bunge hili kulisema hili wazi, vikao vya wadau tumekaa tumekubaliana wakulima wanakopeshwa mbegu na wameshakopeshwa wamelima, safari hii watakopeshwa viuatilifu na mwisho wa msimu kila mkulima atakatwa Sh.150 ili kulipia mbegu walizokopeshwa safari hii jumla ya tani 24,000 na viuadudu na viuatilifu watakavyokuwa wamekopeshwa katika kipindi hiki cha kupulizia dawa. Kwa hiyo, nimtoe hofu kuanzia tarehe 15 wakulima watakuwa katika nafasi nzuri ya kupata dawa husika.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami nimpongeze Hussein Bashe kwa majibu mazuri ya Serikali kwa zao la tumbaku. Tatizo lililoko kwenye zao la Tumbaku ni sawasawa kabisa na tatizo lililoko kwenye zao la Pamba. Mheshimiwa Waziri naelewa unajua tatizo ambalo limewakumba wakulima wa zao la pamba msimu huu, kwa sababu pamba mpaka sasa hivi bado iko kwenye maghala na majumba, Serikali ina utaratibu gani sasa wa kuwasaidia wakulima hawa wanaohangaika na pamba yao ili kusudi msimu ujao tatizo hili lisijitokeze tena? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli zao la pamba kumetokea mtikisiko katika soko la dunia na bei ya pamba katika soko la dunia imeshuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwezi Aprili ilikuwa ni Dollar 0.77 leo iko Dollar 0.60. Kwa hiyo bei imeshuka kwa senti 17 Dollar. Mpaka kufikia leo pamba iliyonunuliwa ni tani 265,000 pamba iliyobaki mikononi mwa wakulima ni tani 90,000. Serikali imechukua jitihada na intervention kupitia Benki Kuu kuweza kujaribu kuongea na mabenki yaweze kutoa fedha kwa makampuni yanayonunua pamba. Hatua ambazo tunachukua za muda mfupi ni hii intervention ya BOT kwa ajili ya kuhakikisha kwamba makampuni yanayoweza kununua pamba yaweze kupata fedha na yatakapokumbana na hasara Benki Kuu iweze kufanya intervention yasipate hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachukua hatua gani, tunapitia upya mfumo wetu wa ununuzi wa pamba, tutahakikisha Serikali ina-regulate kuhakikisha soko ndiyo linalo-determine bei ya kununua pamba na Serikali itasimamia kuhakikisha tunapunguza gharama za uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawaahidi wakulima wa pamba na Waheshimiwa Wabunge, matatizo yaliyojitokeza katika msimu huu katika mazao yote makuu ya kibiashara hayatojirudia katika msimu ujao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. (Makofi)
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, swali hili limekuwa likijirudiarudia kama ulivyosema, lakini nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, na najua Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali sikivu, najua itatekeleza hili kwa sababu ni ahadi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu, kwa sababu wakati wa kuhitimisha bajeti ya Wizara ya Maji, ilituomba sisi Waheshimiwa Wabunge kwa sababu miradi hii mikubwa inachukua muda mrefu, ikatuomba tulete orodha ya pampu au visima vilivyoharibika ambavyo havitoi maji na mimi kama Mbunge wa Jimbo la Sumve nimeshafanya hivyo, nimekuletea Mheshimiwa Waziri. Lini sasa miradi hii midogomidogo ya maji itakamilika na kutekelezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimimiwa Spika, nipende kwa dhati ya moyo kumpongeza Mheshimiwa mkongwe mahili katika kuhakikisha kwamba anapigania wananchi wake katika Jimbo la Sumve. Lakini pia amekuwa funzo kwa hasa hususan kwa sisi viongozi vijana tumekuwa tukijifunza mambo mengi sana katika ujengaji wake wa hoja na hata katika suala zima la ufuatiliaji wa mambo mbalimbali yanayohusiana na maendeleo ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, nataka nimuhakikishie Mhehsimiwa Mbunge, Mheshimiwa Waziri alishatoa agizo kwa maana ya Waheshimiwa Wabunge waliohitaji vizima ama ukarabati walete orodha ile kwa haraka, miongoni mwa Wabunge walioleta haraka ni Mheshimiwa Ndassa, nataka nikuhakikishie kwa uharaka ulioufanya na sisi kama viongozi wa Wizara tutalifanya kwa jitihada kwa haraka ili tuweze kumchimbia visima katika kupunguza shida ya maji katika Jimbo lake, ahsante.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, mbali na Isaka kuwa dry port, stesheni ya Bukwimba ambayo iko Wilaya ya Kwimba tulishaomba kupitia TPA/kupitia TRL. Tunataka kujua sasa Mpango ni lini sasa mpango huo wa kuweka dry port katika Stesheni ya Bukwimba utafanyika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Spika, ahsante, Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Ndassa, Seneta, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na Wizara nzima kwa ujumla, naomba kumpongeza sana Mheshimiwa Ndassa kwa jinsi anavyofuatilia masuala ya miundombinu katika Jimbo lake na nchi nzima kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende tu kumjibu Mheshimiwa Ndassa kwamba eneo la Bukwimba lipo kwenye mipango ya Shirika la Reli pamoja na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari kwa ajili ya kujenga bandari kavu, sasa hivi tunachosubiri ni ile layout plan ya watu wa Wilaya ya Bukwimba ambayo tukishaipata tutaweka layout plan yetu tena ndani ya eneo hilo kwa ajili ya kujenga hiyo dry port.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kwanza niipongeze Serikali kwa kukubali na kupokea ombi la Wilaya ya Kwimba yenye majimbo mawili kwamba itaanza ujenzi huo kwenye mwaka wa fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa sababu Madiwani wa Wilaya ya Kwimba ambao sasa wamesharidhia kama walivyoombwa na VETA wenyewe kwamba ile hati ambayo ilikuwa imeandikwa Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba ihame sasa iende VETA kazi ambayo imeshafanywa na tumeshapeleka hati hiyo kwenda kubadilishwa, nini hatua inayofuata sasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, si vibaya kujua maoteo ya gharama ya ujenzi wa chuo hicho. Je, gharama hiyo ni shilingi ngapi hadi kikamilike?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tunapokea pongezi zake lakini naomba nimhakikishie kwamba pindi wao watakapokuwa wamekamilisha taratibu za kupata ardhi na hati wawasilishe Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili mchakato wa ujenzi uweze kuanza mara moja. Nina hakika utaratibu ukikamilika mradi utasimamiwa vizuri kwa sababu Mheshimiwa Mbunge amebahatika vilevile kuwa na DC mahiri na mzuri sana Mheshimiwa Senyi. Kwa hiyo, nategemea kwamba fedha zile zikipatikana mradi ule utaenda vizuri.

Kuhusu maoteo ya gharama za mradi ule kwa sasa Wizara imefikiria kwamba tutahitaji angalau shilingi bilioni 1.5 kama matumizi ya awali. Hata hivyo, Wizara iko tayari kuweka fedha kwenye mradi kadri mahitaji yatakavyotokea.