Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Richard Mganga Ndassa (1 total)

MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa nafasi hii ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu. Mheshimiwa Waziri Mkuu najua unajua kwamba kwenye msimu huu unaoendelea wa pamba, zao hili limekumbwa na kadhia mbalimbali. Ningependa kujua changamoto hizi, ya kwanza, tani elfu 35 zilizochukuliwa na wanunuzi na wakulimwa wakakopwa, tani 52 elfu ambazo ziko maghalani kupitia AMCOS, ambazo pia wakulima wamekopwa hawajalipwa, tani elfu 70 zinazokisiwa, ambazo ziko majumbani bado hazijapelekwa kwenye soko.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu tungependa kujua, nini kauli ya Serikali au tamko la Serikali kuhusu wakulima wa zao la pamba ambao pamba yao iko majumbani lakini wamekopwa mpaka sasa hivi hawajalipwa? Nini kauli ya Serikali? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika naomba kujibu swali la Mheshimiwa Senator Ndassa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la pamba Serikali tumelifanyia kazi kweli kweli na kwa bahati sasa pamba inalimwa kwenye mikoa zaidi ya 11 nchini na uzalishaji tunafurahi sana kwamba umeongezeka kutoka tani 220,000 mwaka uliopita na msimu huu tumekwenda mpaka tani 300,000, tunategemea kupata tani zaidi ya 350,000.

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali imeendelea kusikia malalamiko ya baadhi ya wakulima kwamba pamba hainunuliwi ni kweli, na sisi tumepita, mimi mwenyewe nimepita, Mawaziri wa Kilimo, Waziri mwenyewe, Manaibu wake wamepita maeneo yote kuona hali hiyo lakini na kuzungumza pia na wananchi kwenye maeneo hayo. Tumekuwa na vikao vya wadau, wadau wanaohusika ni wakulima, wanunuzi, wafanyabiashara na kwa maana ya wanunuzi, watu wa mabenki pamoja na viongozi wa Serikali wa maeneo hayo ili kuona njia sahihi ya kuondoa pamba yote mikononi mwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, nafurahi kusema kwamba, utaratibu ambao tumeuweka wiki tatu zilizopita umeanza kuleta matunda kwamba sasa ununuzi wa pamba tumeshafikia asilimia kama 80 hivi, kwa sababu tumeshanunua tani, mpaka juzi, tani ambazo tumeshanunua ni tani 235,000. Kwa hiyo, pamba ambayo bado iko ni kidogo na kwa hiyo tunaamini kwamba pamba hii yote tutaichukua.

Mheshimiwa Spika, utaratibu tuliouweka kuwahakikishia wakulima kwamba pamba hii tutaichukua, ni kwamba baada ya kuchanganua pamba iliyobaki kwa wakulima tumeigawa kwa wanunuzi maalum ambao wana uhakika wa kuinunua pamba hiyo kwa kilograms zao na tumeshafika mpaka kilograms zote mpaka laki tatu, kila mmoja ana mgao huo na Benki Kuu kupitia mabenki, wanunuzi wale wanapewa fedha za kwenda kuchukua pamba yote mikononi mwa wakulima na zoezi la kuwapa fedha hizo linaendelea na wanunuzi wanakwenda sasa kuchukua pamba.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuna uhakika katika kipindi kifupi kijacho pamba yote itatoka mikononi mwa wakulima na itabaki mikononi mwa wanunuzi ili utaratibu wa kwenda kufanya mauzo uendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri sana juzi tulikuwa na kikao cha pamoja kati ya Benki Kuu, Mabenki na Wawakilishi wa wanunuzi na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge ambao pia walipata fursa ya kuingia pale kwenda kusikia mpango mkakati wa kumaliza pamba yote kule kwa wananchi. Kwa hiyo, niendelee kuwahakikishia wanunuzi wa pamba kupitia Waheshimiwa Wabunge ambao mnatoka kwenye mikoa ile yote kwamba, pamba yote itachukuliwa kwa sababu mpango wa fedha kuwapatia wanunuzi, wanunuzi wakachukue pamba unaendelea na pia tumewashirikisha Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa kwa kuwaambia wilaya yako inanunuliwa na fulani na mnunuzi huyo atachukua kilo kadhaa kwenye eneo hilo na tumeshampa fedha, kwa hiyo, kazi pale ni kushirikiana naye kwenda kuichukua pamba yote ili iweze kuondoka mikononi mwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka niwahakikishie kupitia Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza swali Mheshimiwa Ndassa ambaye pia ni mwakilishi wa wakulima wa pamba kule Kwimba, kwamba pamba yote ambayo tumeizalisha hii, tutaitoa sasa wakati huu tunafikiria kwamba hali ya hewa inaweza kubadilika wakati wowote ili isiweze kunyeshewa na mvua, tuwahakikishie kwamba pamba yote imetoka mikononi mwa wakulima. Ahsante sana. (Makofi)