Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia (38 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi hii, na nimshukuru Mwenyenzi mungu ambaye ameniwezesha afya njema na kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu bila kuwasahau wananchi wa Mtwara Vijijini ambao wameniwezesha kurudi kwa mara ya tatu katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa katika Bunge hili ambayo kwa kweli imegusa katika kila suala. Mimi kwa kifupi kama ambavyo umeshauri, ningependa nizungumzie maeneo machache.
Eneo la kwanza ningependa kuzungumzia suala la viwanda, ambalo Mheshimiwa Rais amesisitiza wakati wote kwamba Serikali yake itakuwa ni Serikali ya viwanda. Naunga mkona sana suala hilo, na napendekeza suala la wapi viwanda vijengwe, tuangalie vigezo vya kiuchumi zaidi. Mwenyenzi Mungu ameiumba nchi yetu kila eneo lipo zao au ipo rasilimali au malighafi ambazo amewajalia.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na Mkoa wangu ambao Mwenyenzi Mungu ameujalia gesi nyingi, ameujalia zao la korosho, bila kusahau bandari ambayo ni ya asili yenye kina kirefu. Kwa hiyo, naunga mkono Wizara ya Fedha na Uchumi ambayo kupitia Mpango wa Taifa wa miaka miwili, mapendekezo waliyoyatoa miaka mitano ijayo ambayo wamependekeza kuendeleza maeneo ya viwanda eneo la Mtwara likiwa ni mojawapo. Ningependekeza na ningeishauri Serikali kwamba suala la uendelezaji wa viwanda liende sambamba na uendelezaji wa miundombinu ambayo itawezesha viwanda vile kufanya kazi kwa ufanisi, ikiwemo reli ya kutoka Mtwara hadi Songea kwenda Liganga na Mchuchuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, reli ile itawezesha sana kubeba malighafi kutoka Liganga na Mchuchuma kuja Mtwara na vilevile kusafirisha bidhaa ambazo zitazalishwa katika viwanda ambavyo vitakuwepo kule Mtwara. Mtwara imejaliwa gesi na sasa hivi bomba la gesi limejengwa hadi Dar es salaam, lakini bei ya gesi ni sawa Mtwara na Dar es Salaam. Wakati ukiangalia bei ya mafuta ni tofauti, Dar es Salaam tofauti na Mtwara, tofauti na Kigoma na tofauti na eneo lingine. Kwa kuweka bei ya gesi sawa Mtwara na Dar es Salaam au Mikoa mingine ndiyo kusema unataka kuua uwekezaji wa Mkoa wa Mtwara. Kwa sababu hakutakuwa na motisha yeyote mtu kwenda kuweka kiwanda Mtwara wakati bei ya gesi popote anapohitaji ataipata kwa bei ile ile. Kwa hiyo, nimuombe Waziri wa Nishati aliangalie suala hilo la bei ya gesi.
Mheshimiwa Naibu Waziri, suala lingine ambalo nataka pia nilizungumzie ni suala zima la uendelezaji wa bandari ya Mtwara na uwanja wa ndege wa Mtwara. Uchimbaji mkubwa wa gesi unafanyika baharini na wafanyakazi wanapelekwa kule kwa helkopta na kurudishwa kwa helkopta na wakati mwingine kama ilivyo katika eneo lolote la kazi wakati mwingine zinatokea ajali kule. Sasa ikitokea usiku ni suala gumu sana kuwaleta wale majeruhi huku nchi kavu kwa sababu uwanja wa ndege wa Mtwara hauna taa. Ukiachia taa ule uwanja ulijengwa mwaka1965, hata mzungumzaji nikiwa sijazaliwa, lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza hakuna ukarabati wa maana uliyofanyika katika uwanja ule, kwa hiyo, niombe Serikali iufanyie ukarabati uwanja ule uendane na uwekezaji ambao uko kule.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia suala zima la viwanda vya korosho na suala zima la ukamilishaji wa hospitali ya Rufaa katika Mkoa ule. Pia suala la maji, viwanda vyote vinahitaji maji, wananchi wanahitaji maji, lakini shughuli za binadamu nyingi zinahitaji maji. Ningependa kurudia tena kwamba suala la uwekezaji wa viwanda uende sambamba na uwekezaji wa miundombinu ambayo inabeba au inawezesha viwanda vile kufanya kazi ikiwemo umeme, barabara, reli, bandari, hospitali kwa sababu wafanyakazi pia wanahitaji kuwa na afya ili waweze kutumika vyema.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hotuba ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema zake ikiwemo uzima na afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba ambayo pia ameisoma kwa umahiri mkubwa sana. Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ya Viwanda, napenda kuishauri Serikali kama tunataka kufikia lengo hili kwa ufanisi ifuatavyo:
Maeneo yote ya EPZA na SEZ ambayo hayajalipiwa fidia yakiwemo ya Kurasini, Bagamoyo na Mtwara wahakikishe kuwa fidia hiyo inalipwa kwa wakati na kusafishwa ili wawekezaji wasipate usumbufu juu ya upatikanaji wa ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la miundombinu wezeshi, umeme wa uhakika, barabara na reli ni muhimu sana ili kuhakikisha tunazalisha bidhaa ambazo zitaweza kushindana na bidhaa nyingine kutoka nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kupata majibu kutoka kwa Waziri kuhusu suala la kiwanda cha Mbolea Msangamkuu Mtwara, ningependa kufahamu ni lini kiwanda hicho kitapatiwa uhakika wa kupewa gesi ili kiwanda hicho kianze kujengwa ninafikiri kushika shilingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka kweli kuwa nchi ya Viwanda, Serikali yangu ni lazima tuweke sheria za maksudi kwa ajili ya kulinda viwanda vyetu. Nchi yetu ina uwezo wa kuzalisha alizeti na mafuta ya alizeti na kulisha Afrika Mashariki, lakini tunashindwa kwa sababu ya mafuta ya kutoka nje ambayo hatuna hata uhakika wa usalama wa afya zetu. Naomba Serikali iondoe usumbufu kwa wawekezaji, tuangalie sheria zetu za kodi, utaratibu wa kupata ardhi kwa wawekezaji na kuthubutu kutoa maamuzi kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, viwanda vya korosho ni muhimu sana kwa maendeleo ya wakulima wa korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Kabla ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia afya na uzima wa kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na kuweza kuichangia hotuba ya Wizara ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kumpongeza sana Waziri wa Afya pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri sana wanayoifanya. Ndani ya muda mfupi wameweza kutembelea mikoa mbalimbali na kuweza kutoa maelekezo mbalimbali, hali ambayo pia inawatia moyo hata watendaji wanaofanya kazi katika Sekta hii ya Afya. Hongereni sana na mwendelee kuchapa kazi hivyo hivyo na msimwangushe Mheshimiwa Rais. Nyie ni vijana na tunawategemea, mna nguvu pia mnao uwezo mkubwa sana, endeleeni kuchapa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia katika maeneo makuu matatu. Kwanza, namwomba Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, maeneo makuu matatu ambayo ni changamoto sana katika Sekta ya Afya; kwanza ni upatikanaji wa madawa na vifaa tiba; pili, ni suala la miundombinu ya kutolea huduma; na tatu, ni uchache wa watumishi katika Sekta ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la upatikanaji wa madawa na vifaa tiba ni imani yangu kwamba Wizara ikidhamiria, ikiweka fedha za kutosha, ni suala ambalo linaweza likatatuliwa hata ndani ya miezi sita. Ni suala la dhamira tu, Serikali ikiamua inaweza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija katika suala la miundombinu, sasa hivi pamoja na juhudi zote zinazofanyika, lakini katika baadhi ya maeneo, miundombinu iliyopo kwa kweli imechoka na pia imeelemewa kutokana na idadi ya watu inayoongezeka kila siku, mfano mzuri ni Muhimbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni miongoni mwa wanaoiamini hospitali ile kuliko hospitali nyingine zote katika nchi yetu. Ukienda pale, idadi ya wagonjwa ukilinganisha na idadi ya wodi pamoja na vitanda kwa kweli inatia huruma. Unawahurumia hata Wauguzi na Madaktari. Wagonjwa wanalala chini kwa sababu wodi ni chache, hata ukiongeza vitanda hakuna eneo ambalo unaweza ukaweka. Ifike wakati sasa suala la ujenzi wa hospitali ya Mlonganzila kwa kweli lipewe kipaumbele kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tunazo hospitali zetu za Kanda zipewe uwezo kwa maana ya Watendaji na vifaa ili ziweze kusaidia Muhimbili kupunguza mlundikano. Kwa upande wa kusini, Mikoa ya Mtwara na Lindi, tunayo Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kusini ambayo inajengwa pale Mikindani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia katika Bajeti yako Mheshimiwa Waziri, sijaona eneo lolote. Nimeangalia kwenye bajeti ya maendeleo, nimeona Hospitali ya Rufaa Mtwara shilingi bilioni mbili. Sasa sijui zile shilingi bilioni zinakwenda Ligula au zinakwenda Mikindani! Kwa sababu kama ni Mikindani, Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kusini, shilingi bilioni mbili kwa kweli hazitoshi, kwa sababu mpaka sasa hivi kilichojengwa pale ni majengo ya wagonjwa wa nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka kweli tuisaidie Muhimbili ni lazima tuhakikishe zile Hospitali za Rufaa za Kanda zinajengwa na zinawezeshwa. Sasa hivi mgonjwa yeyote pale Ligula akishindikana, inabidi asafirishwe kwenda Muhimbili. Wakati mwingine Mheshimiwa unalazimika kama Mbunge kununua viti sita kwenye ndege ili mgonjwa mmoja tu aweze kusafirishwa. Afadhali ikiwa ATC, shilingi milioni unaweza ukasafirisha mgonjwa, lakini ukija kwenye Precision, mpaka shilingi milioni 15 kusafirisha mgonjwa mmoja. Kwa kweli kwa wale ambao hawana uwezo hawawezi; na wakati mwingine hata Mbunge huwezi kutoa shilingi milioni 15 kusafirisha mgonjwa mmoja. Tunaomba hospitali ile ijengwe na iweze kukamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwa upande wa watumishi, tuna vituo vya kutolea huduma zaidi ya 7,249 ukichanganya na sekta binafsi, lakini na mahitaji ya watumishi kwa upande wa Wauguzi ni zaidi ya 46,000 na waliopo ni kama 24,000. Tuna upungufu wa zaidi ya asilimia 49 ya watumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika udahili wa watumishi wetu; nilikuwa naangalia, unakuta Madaktari kwa mwaka wanadahiliwa 1,670 wakati tuna upungufu wa Madaktari zaidi ya 4,000. Kwa upande wa Wauguzi, tuna upungufu wa Wauguzi zaidi ya 22,000, lakini wanaodahiliwa kwa mwaka ni kama 3,499. Hivi kweli tunaweza tukaondoa tatizo hili? Tulikuwa na tatizo la Wahasibu na tatizo la Walimu, Wizara mama zilikuwa zinatenga kiasi cha kutosha ili kuweza kuondoa matatizo haya. Sasa hivi tatizo la Walimu na Wahasibu ni kama limekwisha lakini kwa upande wa Sekta ya Afya, nawaomba wadogo zangu, Mheshimiwa Ummy na Mheshimiwa Kigwangalla ni lazima tuje na mpango mahsusi, tupanue vyuo vyetu vya Wauguzi, Madaktari na kada zote za Sekta ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni lazima tuwalipie. Serikali itenge pesa kama ambavyo Wizara ya Fedha ilikuwa inatenga pesa kwa ajili ya Wahasibu; kama ambavyo Wizara ya Elimu na Wizara ya Kilimo zilikuwa zinatenga pesa kwa ajili ya kusomesha watumishi wao. Ni lazima Wizara ya Afya tufanye kama operation. Tunasema anayekwenda kuchukua degree ya Uuguzi atachukua mkopo, lakini wanaokwenda kuchukua Cheti, Diploma tunasema ajitegemee mwenyewe. Karo yenyewe ni zaidi ya shilingi milioni moja. Chakula kinazidi hata hiyo shilingi milioni moja. Kwa kweli kama tunataka kuondokana na upungufu huo, nimwombe Mheshimiwa Waziri, ni lazima tuwe na mpango mahsusi na tuwekee kipaumbele, tutenge pesa za kutosha kuhakikisha tunadahili vijana wa kutosha hasa wale ambao tunawahitaji kule vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani kwa sisi tunaoishi vijijini, unakuta zahanati moja ina mtumishi mmoja, kule Muuguzi anafanya kazi masaa 24, hana Jumamosi, hana Jumapili; kukiwa na mgonjwa saa 5.00 za usiku anakwenda kuamshwa na sidhani kama kuna chochote wanachokipata. Ndiyo maana unakuta Wauguzi wetu wakati mwingine wanakuwa na lugha zisizostahili. Siyo kwamba wanapenda, ni uchovu wa kazi. Mzigo ni mkubwa wanaoufanya. Kwa hiyo, mtu mmoja halali, usiku kucha anaitwa kazini, asubuhi yuko kazini, Jumamosi yuko kazini, hivi unategemea awe na lugha nzuri? Wakati mwingine ni stress tu kutokana na uzito wa kazi ndiyo unaowafikisha wanakuwa na lugha wengine zisizostahili.
Kwa hiyo, kwa kweli lazima tuongeze udahili, hizi tunazosema kila kijiji kiwe na zahanati, kila kata iwe na kituo cha afya; bila kwenda sambamba na udahili, hizo zahanati na vituo vya afya zitakuwa ni nyumba tu za popo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nichangie, nirudi katika Mkoa wangu. Tunacho Kituo cha Afya cha Nanguruwe ambacho tulikiombea kuwa Hospitali ya Wilaya. Tumekamilisha karibu mahitaji yote yanayotakiwa. Tunayo majengo ya upasuaji, tunavyo vitanda vya kutosha, wodi za kutosha pamoja na Kituo cha Afya cha Nanyumbu; lakini mpaka sasa hivi bado tunasubiri kibali kutoka Wizarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ummy alikwenda kutembelea Kituo cha Afya cha Nanguruwe, nina imani kabisa kwamba yeye mwenyewe amejiridhisha kwamba vipo vifaa vya kutosha na majengo ya kutosha. Tunaomba watoe kibali ili ianze kufanya kazi kama Hospitali ya Wilaya, tupunguzie mzigo hospitali ya Mkoa ya Ligula. Hii ikienda sambamba na hospitali au Kituo cha Afya cha Nanyumbu ambacho nacho kwa muda mrefu kimeshafikia mahitaji ambayo yanatakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Mtwara Vijijini tunavyo vituo vya afya vya Mahurunga na Kitere. Tumeshajenga vyumba vya upasuaji; vifaa vyote vipo kwa zaidi ya miaka miwili, lakini hakuna huduma inayotolewa pale, tatizo ni lile lile la uchache wa Madaktari. Nakuomba Mheshimiwa Waziri utuletee Madaktari wa kutosha ili vituo vile vianze kutoa huduma ya upasuaji na tuweze kupunguza vifo vya akinamama na watoto hasa wakati wa kujifungua. Pia Mheshimiwa Waziri, wakati unaoandaa hao Madaktari, tunao Madaktari pale Hospitali ya Mkoa ya Ligula.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo tatizo katika Wilaya yetu na hata kwa mkoa wetu suala la Mabusha. Kwa vile katika vituo vile huduma zote zipo, vifaa vyote vipo, kwa nini hao Madaktari wasiwe wanapanga siku angalau kwa wiki au kwa mwezi wanakwenda katika Vituo vya Afya vile ambavyo vina huduma za upasuaji, wakawa wanatoa huduma ile kwa wale ambao wanahitaji kufanyiwa operation za mabusha? Kwa sababu sasa hivi wanalazimika kuja katika Hospitali ya Mkoa, tunawagharamia, anafika pale anakaa zaidi ya wiki mbili anasubiri zamu. Mara leo sijui tunafanyia wawili, kesho tunawafanyia watatu; kwa nini wale Madaktari walioko katika mkoa wasiwe wanazunguka na wanakwenda katika maeneo hayo kutoa huduma? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napendekeza kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake ni suala la uzazi wa mpango. Nimeangalia katika kitabu cha hotuba haraka haraka, sikuona eneo lolote lililozungumzia suala la uzazi wa mpango. Suala la idadi ya watu na uchumi wa nchi yetu ni muhimu sana. Maeneo mengine kama Wabunge tukienda kule wanatuambia bwana hizi huduma hatuzipati na wanazihitaji. Unakuta kule akinamama wengine tayari ana watoto 10 na uzazi wake ni wa matatizo, ni lazima ajifungulie katika hospitali ya Mkoa. Kwanini wasishauriwe uzazi wa mpango sahihi kwa ajili ya kuwawezesha na wenyewe kuboresha afya zao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine wanapoteza maisha kwasababu tu kila baada ya mwaka mmoja ana mtoto au unakuta mtu tayari ameshajifungua kwa zaidi ya mara nane hali ambayo ni kihatarishi cha maisha yake kwa sababu kwa kweli baada ya kuzaa kwa zaidi ya mara nane, nadhani Mheshimiwa Kigwangalla, Naibu Waziri wa Afya ananielewa, ni kwamba kila kizazi kinachoongezeka pale ni hatari kwa maisha ya mama yule anayejifungua na hata mtoto anayejifungua. Ukiangalia vifo vingi vinavyotokana na uzazi ni aidha ni vya wale waliojifungua katika umri mdogo au kwenye umri uliopitiliza umri ule ambao kwa kweli mtu anaweza akajifungua salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusisitiza suala la Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini. Mheshimiwa Waziri akapokuja tungependa kusikia bajeti yake imetengwa wapi. Kama tunataka kupunguza vifo vya akinamama na watoto, tuangalie suala zima la magari ya wagonjwa. Siku za nyuma tulikuwa na magari ya wagonjwa, yana radio call ndani yake, kukiwa na tatizo wanaweza kuwasiliana kwa radio call na gari lolote lililoko karibu na eneo ambalo mgonjwa yupo linaweza likaenda kumchukua kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza kwa Mheshimiwa Waziri kwamba sasa hivi tuwe na magari ya wagonjwa ambayo pia ni surgical. Mgonjwa anapofuatwa, basi afuatwe na Daktari na akifika siyo kwenda kumchukua na kumkimbiza zaidi ya kilometa mia moja Makao Makuu ya Wilaya au ya Mkoa kwa ajili ya upasuaji. Gari ikifika, aweze kufanyiwa upasuaji kule kule inakomkuta badala ya kuanza kukimbizana naye. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kujua hilo, kama tunao mpango wa kuwa na magari ya wagonjwa ambapo huduma za upasuaji zinaweza kupatikana humo humo ndani ya magari kama ambavyo nchi nyingine zinafanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsanteni sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. HAWA A. GHASIA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA BAJETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kutolea ufafanuzi hoja mbalimbali ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge, ambao baadhi yao wamezileta kwa maandishi idadi yao ni nane na baadhi yao wametoa kwa kuzungumza ambao idadi yao inafikia 14 ikiwa na pamoja Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tuna tatizo la muda, naomba niende moja kwa moja katika hoja ambazo zimezungumzwa. Nianze na Mheshimiwa Riziki Lulida ambaye amezungumzia uwepo wa rasilimali na akaomba kwamba Serikali izisimamie rasilimali hizo ili kuhakikisha kwamba zinaleta tija katika Taifa letu. Nakubaliana naye na sina haja ya kuendelea kuijadili hoja hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Riziki Lulida pia aligusia pia suala la zao la korosho haswa akijikita katika eneo la uhujumu wa zao hilo, kwa kile kitendo ambacho korosho zetu zilizokwenda Vietnam kugundulika kuwa na mawe na masuala mengine. Mheshimiwa Naibu Waziri, Dkt. Mary Mwanjelwa amelitolea ufafanuzi lakini bado tunaendelea kusisitiza, naungana na Mheshimiwa Riziki Lulida kwamba bado Serikali inatakiwa ichukue hatua mbalimbali kuhakikisha kwamba suala hilo halijotokezi tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sisi ambao tunatoka katika maeneo ya korosho tunaona kitendo hiki kama hujuma kwa wale wanunuzi wapya ambao wamejitokeza katika zao hili na kuwezesha kupandisha bei na hata kufikia Sh. 4,000/= kwa kilo. Kwa sababu wapo ambao walikuwa wananufaika na bei zile za chini ambazo zilikuwa zinawanyonya wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunahisi kuongezeka kwa bei za korosho ambako kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na uwepo wa wanunuzi kutoka nchi za Vietnam, Uturuki na China kunaweza kukawa ni sababu ya kuwafanyia hizi hujuma ili kuwakatisha tamaa wasiweze kuja kununua korosho zetu na hivyo kushusha bei za korosho.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunasisitiza suala la kuchukua hatua thabiti kwa wale waliohusika lakini pia kama Serikali iwekeze kwa kujenga maghala ambayo yataweza kuhakikisha kwamba muuzaji wa korosho anavyopeleka pale, tukiwa na maghala yanayokubalika, kwa utaratibu wa ununuzi wa korosho huwa zinamwagwa na hivyo kuhakikisha kwamba zinakaguliwa kabla ya kusafirishwa kwenda kule kwa wanunuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tukiwa na viwanda ambapo wale wawekezaji watakuja kubangua hapa hayo masuala mengine nadhani yataweza kuthibitiwa. Pia kwa upande wa Mkoa wa Mtwara, ilishapendekezwa kwamba korosho zote zinazozalishwa Mtwara na Lindi zitumie bandari ya Mtwara ili kuweza kudhibiti suala hili la kuziharibu korosho zetu zikiwa njiani zikielekea bandari ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hizi korosho ambazo zimeonekana kuwa na mawe, baada ya kuzifuatilia ni zile korosho ambazo zimesafirishwa kupitia bandari ya Dar es Salaam. Kwa hiyo, tunarudia tena kusema kwamba hatua sahihi zichukuliwe kwa wale wote waliohusika kuharibu ubora wa korosho zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mzungumzaji wa pili ni Mheshimwa Balozi Diodorus Kamala ambaye aliomba suala la 10% kwenye mafuta ya kula kutoka nje liendelee na pia kusaidia sekta ya ngozi kama ambavyo wenzetu Ethiopia wanavyofanya. Tunaungana naye mkono hakuna haja ya kubishana naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mzungumzaji mwingine ambaye alichangia kuhusu Kamati yetu ni Mheshimiwa Lolesia Bukwimba ambaye alisisitiza suala la Serikali kulipa madeni yote ya ndani na pia kufanyia marekebisho Sheria ya Manunuzi na pia kuziwezesha taasisi kimitaji ili ziweze kutekeleza majukumu yake. Naungana naye mkono katika hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Jitu Soni aliiomba Serikali kufanya tathmini ya gharama za uzalishaji ikiwemo tozo zinazotozwa na Mamlaka zetu za Udhibiti nadhani Mheshimiwa Waziri amelijibu, kwa hiyo, sina haja ya kulirudia. Pia mifumo ya malipo iendelee kuimarishwa ambalo pia Kamati tumelishalisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa David Silinde alizungumzia suala la urahisi wa ufanyaji wa biashara na uwekezaji. Pia alizungumzia kwamba tumeporomoka katika maeneo saba. Katika taarifa yangu nilisema tunaipongeza TAMISEMI pamoja na Wizara ya Ardhi, walikuja na maeneo ambayo yamewasababishia kuporomoka na wakaja pia na mikakati thabiti waliyoiweka na ambayo sisi kama Kamati tuliridhika. Bado tunaendelea kuisisitiza Wizara ya Viwanda na Biashara kuweka mikakati thabiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri amesema kwamba wanayo Blue Print lakini Blue Print ni maandishi yaliyopo na tumekuwa nayo muda mrefu. Tunaomba hiyo Blue Print ifanyiwe kazi kuhakikisha inaleta tija. Kwa hiyo, nimwombe shemeji yangu Mheshimiwa Mwijage apunguze maneno aongeze vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Janet Mbene alizungumzia suala la magogo kutoka Congo na pia tupate mikakati ya kuinua uchumi wetu na pia pongezi ambazo alizitoa kwenye Mfuko ya Kahawa katika kuondoa tozo za Kahawa na pia kupendekeza tozo zingine ambazo zitawalenga wakulima wetu. Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana naye sana kwa hayo aliyozungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzanite yetu inasafirishwa kwa wingi na nchi jirani lakini sisi nchi jirani zikitaka kuleta biashara zao kama magogo au korosho kutoka Mozambique kuleta Tanzania wauze huku kwetu tunakuwa na vikwazo vingi. Kwa hiyo, tuiombe Serikali iondoe vikwazo, hivi korosho ya kutoka Kaskazini Mozambique ikiuzwa Mtwara na Mtwara ndiyo wakasafirisha kwenda nje, kuna tatizo gani?

Magogo kutoka Congo yakisafirishwa kupitia bandari ya Tanzania au yakiuzwa Tanzania kuna tatizo gani? Kwa hiyo, tuangalie uwezekano wa kuondoa hivyo vikwazo ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Hussein Bashe alitoa mapendekezo yake na pia alisisitiza suala la viwanda vyetu pia kuoanishwa na sekta ya kilimo ambayo inaajiri kwa kiasi kikubwa Watanzania. Tunaomba Serikali hilo ilifanyie kazi. Pia aliongelea kuweka vivutio ambavyo vitasaidia viwanda vilivyoko nje kuja kuwekwa huku ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Halima Mdee alizungumzia suala la kunyang’anya vyanzo vya mapato vya Halmashauri na kwamba pesa nyingi zilizoenda katika Halmashauri zimeenda kulipa madeni. Serikali eneo hili imelijibia lakini pia tukumbuke tunavyoandaa bajeti zetu huwa tunaweka na bajeti ya kulipa madeni na wazabuni. Kwa hiyo, sioni tatizo tukisema kwamba pesa zilizokwenda zimeenda kulipa madeni zaidi kwa sababu bajeti pia ilikuwa inasema hivyo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Mheshimiwa Sixtus Mapunda kwamba ATCL itazamwe na iwezeshwe, tusiangalie tu suala kwamba inaleta faida kiasi gani kwa maana ya pesa ile ya kuiona moja kwa moja, hapana, tuangalie faida za ujumla. Kwa kweli ATCL ina mchango mkubwa sana katika kuinua uchumi wetu na hasa katika sekta za utalii lakini pia hata kuharakisha usafirishaji na kuwezesha uwekezaji katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niungane na wale wanaosema kwamba tuziangalie taasisi zile ambazo zina mwingiliano ili kuondoa kero za kikodi na zisizo za kikodi kama vile TFDA na TBS ikiwezekana iunganishwe na iwe taasisi moja ambayo inatoa huduma zote hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri, Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa kwa zile ahadi alizoahidi tunaomba basi ziharakishwe na hatua zichukuliwe.

Mheshimiwa Ashantu Kijaji, tunakubaliana naye, sina haja ya kurudia kule lakini nirudie kwa Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara. Mheshimiwa Rais alishatoa maelekezo kwamba viwanda vyote vilivyobinafsishwa na ambavyo havifanyi kazi yake iliyokusudiwa virudishwe mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vya korosho karibu vyote, vingi viliuzwa kwa milioni 50 na vingine waliouziwa hawakutoa hata senti tano. Sasa hivi viwanda vile vimegeuzwa kuwa maghala wanawakodisha wakulima kwa kuhifadhi korosho zao mle ndani. Nimwombe Mheshimiwa Charles Mwijage, Waziri wa Viwanda na Biashara atekeleze agizo la Mheshimiwa Rais, la kuhakikisha viwanda vile ambavyo vilibinafsishwa kwa bei nafuu zaidi ambapo wale wawekezaji wameacha kufanya yale majukumu ambayo waliagizwa basi vinarejeshwa kama Mheshimiwa Rais alivyoagiza. Kama Rais alimeshaagiza kigugumizi ni cha nini ndugu zangu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe tena kwa wenzetu Wizara ya Fedha waangalie zile tozo ambazo wamepunguza lakini kama zipo tozo ambazo wanaziona ni kwa manufaa ya nchi yetu na Serikali yetu basi pia tuendelee kuzipunguza ili kuhakikisha kwamba tunaweka mazingira bora ya kufanyia biashara na kuvutia uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirejee tena kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi kuja kutoa ufafanuzi katika hoja zile ambazo zimechangiwa na Waheshimiwa Wabunge na pia niishukuru sana Kamati yangu ya Bajeti kwa kazi kubwa ambayo tumeifanya katika kipindi chote cha uhai wa Kamati. Niishukuru pia Sekretarieti, nimshukuru Katibu wa Bunge kwa kuiwezesha Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja sasa kwamba mapendekezo yote yaliyotolewa na Kamati yakubaliwe ili yaweze kutekelezwa na Serikali iyafanyie kazi pia na Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye amenijalia afya na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na kuweza kuchangia Muswada huu wa masuala ya huduma za habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuweza kuuingiza Muswada huu Bungeni baada ya zaidi ya miaka 20 pamoja na vikwazo mbalimbali ambavyo vimejitokeza. Kwa hiyo, nampongeza sana Waziri na Naibu wake pamoja na Maafisa wa Wizara yao kwa kazi kubwa sana ambayo wameifanya kuhakikisha Muswada huu unaingia ndani ya Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda nichukie fursa hii kumpongeza Mwenyekiti wa Kamati iliyoshughulikia Muswada huu. Kwa kweli wamefanya kazi kubwa sana na katika mazingira magumu. Pia niwapongeze wadau wa habari ambao kwa kweli wamekubali kutoa maoni yao na kuweza kwa kiasi kikubwa kuboresha Muswada huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni masuala ya kawaida Muswada kuandaliwa na Serikali na kuupeleka kwa wadau na kwenye Kamati. Lengo la Serikali kupeleka kwa wadau na kwenye Kamati ni kuhakikisha kwamba wadau wanatoa maoni yao, yale maeneo ambayo wanaona yana upungufu wanayazungumzia ili Serikali iweze kuyarekebisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni suala la ajabu sana Muswada ambao umekaa zaidi ya miaka 20 mdau kila siku ukiambiwa unasema muda hautoshi. Hivi tunao Muswada wowote ambao umejadiliwa zaidi ya miaka 20 ndani ya Bunge hili? Ndiyo maana nawapongeza wale wadau ambao kwa kweli hawakukubali kuburuzwa na hao ambao wamekusudia kuwaburuza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Waziri na Serikali kwa ujumla kwa kufuta kifungu cha 50(4),(9),(10) na (11) ambavyo vilikuwa vinaruhusu polisi kuchukua mashine au mitambo iliyohusika katika kuandika habari ya uchochezi. Hii inaonesha kabisa kwamba Serikali na Waziri wametambua mabadiliko ya teknolojia. Kwa sababu katika mabadiliko ya sasa ya teknolojia, mmiliki wa mtambo anaweza akauweka mtambo wake automatic na mchapishaji akaandika taarifa yake akaleta softcopy kwa ajili tu ya kuchapisha na mmiliki wa mitambo ule asiwe na nafasi ya kusoma lile chapisho mwanzo mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kumchanganya na yeye kwenye makosa kwa kweli naona haikuwa sahihi, lakini naipongeza Serikali yangu kwa kupokea maoni ya wadau na kuviondoa vipengele vyote vinavyohusiana na kuchukua mitambo ambayo imehusika katika kuandika chapisho lenye uchochezi au ambalo kwa kweli linaleta madhara kwa baadhi ya wananchi. Hiyo yote imetokana na mapendekezo ya wadau, Kamati na usikivu wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naamini kabisa kwamba Muswada huu ni mzuri na unalenga kuboresha tasnia hii ya habari. Pia unalenga kulinda haki na wajibu wa vyombo vya habari. Hakuna haki isiyokuwa na ukomo, lazima tasnia kama hii ipewe haki, lakini pia ipewe ukomo na mipaka, ihakikishe haki hiyo wanaitumia vizuri bila kuathiri usalama wa nchi, bila kudhuru wengine na bila kukashfu wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi hapa Tanzania ni mashahidi, Rwanda imeingia katika machafuko na miongoni mwa sababu ni pamoja na uchochezi wa vyombo vya habari. Ndiyo maana mmiliki mmoja wa vyombo vya habari ni miongoni mwa waliohukumiwa kufungwa. Kwa hiyo, tasnia hii hatuwezi tukaicha tu ielee yenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muswada huu kwa kiasi kikubwa, ndiyo maana naipongeza Serikali yangu, unalenga kuwatetea na kuwasaidia waandishi wa habari. Ukiangalia katika kifungu cha 21 Muswada unaanzisha Mfuko wa Mafunzo ya Habari. Sasa kama Muswada unaanzisha Mfuko kwa ajili ya kumwendeleza mwandishi wa habari na tasnia ya habari, hivi unasimamaje mwanasiasa mwenzangu ukasema kwamba Muswada huu unakusudia kuua sekta ya habari au uhuru wa habari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kifungu cha 10 cha Muswada huu inaanzishwa Bodi ya Ithibati ya Wanahabari. Katika kifungu cha 12 kazi za bodi hiyo zimeainishwa ambapo mojawapo ni kutoa ithibati kwa wanahabari, kusimamia kanuni na maadili za nidhamu miongoni mwa wanahabari na kusimamia viwango. Haya ni mambo ya kawaida kwenye taaluma mbalimbali. Hatujaanza na taaluma/tasnia ya habari kwani Bunge hili hili limeshapitisha kuwa na bodi kama hizi kwa Wahasibu (NBAA), tunayo Bodi ya Wahandisi, Bodi ya Wakadiriaji Majengo, Chombo cha Wanasheria, Baraza la Madaktari, Mafamasia, Wauguzi, Wakemia, hiyo ni mifano michache tu. Sasa kama taaluma nyingine zinasimamiwa kwa nini taaluma hii nayo isisimamiwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nipingane na wale wenzangu wanaosema kwamba enzi hizo mtu alikuwa anaajiriwa kuwa mwandishi wa habari bila hata kusomea. Hivi jamani hii nchi baada ya miaka 50 bado tunataka tuendelee kuajiri bila kusomea, yaani mtu atoke chuoni leo aende akawe Mkurugenzi wa Habari Maelezo au mtu bila kusomea hata kidato cha sita hajafika unataka na yeye awe mwandishi wa habari bila cheti, kwa kweli hapana. Ni lazima tuzingatie viwango, lazima tuweke viwango, lazima tuondokane na makanjanja na lazima tuwape heshima wale ambao wamepoteza muda, rasilimali zao kwa ajili ya kujiendeleza katika tasnia hii ya habari, uwatofautishe na wale wanaoandika kwa mazoea tu, lazima tuweke madaraja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukienda katika utumishi wa umma Serikali ilikuwa inaajiri darasa la saba, form four ambaye hana cheti hana chochote hata mimi mwenyewe nimeanza kazi mwaka 1992, fresh from school, form six nikaajiriwa kama PCA (Planning and Controller Assistant) cheo hicho hakipo. Kwa hiyo, tusilazimishe mambo ya miaka 20 leo tuendelee kuwa na watu wa aina hiyo. Enzi hizo wakati watu wanatoka Makerere Tanzania hatukuwa na Chuo cha Uandishi wa Habari hata kimoja chenye kutoa digrii, sasa hivi vimejaa, wasomi wamejaa bado tuendelee na watu wa darasa la saba kuwaita waandishi wa habari? Kwa kweli ni kuidhalilisha tasnia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Muswada huu narudia tena kusema kwamba una lengo la kuwasaidia waandishi wa habari. Katika kifungu cha 58 kinataka kila mwajiri kuweka bima na hifadhi ya jamii kwa kila mtu aliyeajiriwa katika chombo cha habari husika. Wenyewe ni mashahidi, tunao waandishi wetu wa habari wengine wanafikia mpaka kufariki amefanya kazi kwenye chombo zaidi ya miaka sita hana ajira, bima na hajalipiwa kwenye Mfuko wowote wa Hifadhi ya Jamii. Tunao waandishi wa habari wanapata ajali hawana hata bima, hawawezi hata kutibiwa, wengine mpaka wanapata ulemavu wa kudumu hakuna hata bima ya kuwasaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli napenda niipongeze Serikali yangu kwa kuliona hili na kuja na sheria inayowatetea waandishi wa habari. Kwa sababu ukisema awekewe bima na alipiwe hifadhi ya jamii ndiyo moja kwa moja unamaanisha kwamba huyu ni lazima atakuwa na mkataba unaoeleweka, unaomwezesha kulipwa mshahara unaojulikana na sehemu ya huo mshahara ukamlipie kwenye Hifadhi ya Mifuko ya Jamii. Kwa kweli nashangaa kusikia kwamba eti kwa kuwa na hiyo bima na kulipiwa hifadhi ya jamii unanyanyasa, unadidimiza sekta ya habari. Waswahili wanasema ukistaajabu ya Musa utaona ya Firauni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muswada huu katika kifungu cha 21 kama ambavyo nilisema kinaanzisha Mfuko wa Mafunzo ya Wanahabari ambao utaweza kutoa mafunzo kwa wanataaluma ya habari, kukuza programu za uendelezaji maudhui ya ndani ya nchi na kukuza na kuchangia utafiti wa maendeleo katika nyanja za habari na mawasiliano ya umma. Hivi Mwenyezi Mungu awape nini wanahabari? Mie kwa kweli nasema huu Muswada kwanza hatukutakiwa hata tuujadili kwa siku mbili, tungeweza kuujadili kwa siku moja, tukaumaliza ili wenzetu wanahabari nao wajione wako sawa na wanataaluma wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilishangaa sana namsikia mwanahabari anasema eti mnatutaka tuvae suti wakati tunaenda kuandika habari. Ndugu zanguni huu Muswada tunavyoandika au tunavyopitisha sheria lazima tuangalie na sheria nyingine za Kimataifa zinasemaje? Sisi kama nchi tunayo makubaliano mbalimbali ambayo tumeingia na mojawapo ni makubaliano ya Mkataba wa Geneva wa kuwalinda raia na waandishi wa habari katika operesheni mbalimbali au katika maeneo ya vita. Sasa utalindwaje kama hutofautiani na watu wengine?
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuvaa mavazi rasmi katika maeneo maalum ni kwa lengo la kuwalinda wanahabari wenyewe. Usiangalie leo unaandika katika mazingira ya amani, unaweza ukapelekwa Sudan huko ukafanye coverage, lakini kwa vile umeshazoea huku kwenu hakuna kuvaa uniform eneo lolote hata katika mazingira magumu utafika kule utachekesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala hili linalenga kuwalinda wenyewe waandishi wa habari katika mazingira maalum. Kwenye operesheni za polisi, kijeshi hivi wewe usipovaa vazi rasmi la kukutofautisha, siyo kwamba kila siku uwe umevaa hiyo sare lakini katika mazingira maalum, Serikali ina wajibu wa kukulinda mwandishi wa habari usidhurike. Sasa itakulindaje kama haiwezi kukutofautisha na vibaka wengine na wale ambao wamekusudiwa kwenda kufanya operesheni. Kwa hiyo, ili iweze kukutofautisha na wengine na iweze kukulinda ni lazima ikuweke katika vazi linalokutofautisha. Tunaposema vazi siyo lazima iwe uniform chini juu hata ukivaa reflector ni vazi maalum.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kweli nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na Kamati yake pamoja na Uongozi wote wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo kwa kweli niliona nilizungumzie ni kwamba, kwa mtazamo wangu, Muswada huu unampunguzia sana Waziri mamlaka kuliko ambavyo watu wanafikiri. Kwa sababu zamani Waziri mwenyewe alikuwa anaweza kufungia magazeti, chombo cha habari, lakini kwa Muswada huu masuala karibu yote ya kitaaluma yatapelekwa kwenye bodi na Waziri atabaki na masuala machache tu yanayohusiana na uchochezi, amani au usalama wa nchi. Kwa hiyo, siyo kweli kwamba Muswada huu unakusudia kukandamiza tasnia ya habari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe tu wenzetu, kama kweli tumekuja hapa kuwatetea wananchi wanyonge tuungane kuhakikisha kwamba Muswada huu unapita kwa sababu unawalinda sana waandishi wa habari. Hata hivyo, kama nyuma ya pazia kuna mtu ametutuma kuja kumtetea ili hao waandishi wa habari wasiolipwa mishahara, wasiokuwa na mikataba, wasiolipiwa bima waendelee kunyanyaswa, hebu mkae ninyi wenyewe mzungumze ndani ya nafsi yenu, mumwogope Mwenyezi Mungu. (Makofi)
Haiwezekani mtu awe na chombo cha habari, ameajiri watu hawana mshahara, hawana bima anawalipa anavyotaka yeye.Kwa kweli huo siyo uhuru wa habari tunaoutaka, tunataka uhuru ambao pia unajali maslahi ya wale wanaoleta habari.
Mheshimiwa Sugu hata kama inauma vumilia, hata kama sindano imeingia imekuchoma vumilia ndiyo uanaume. Watakaposimama wanaume wenzako utafanyaje kama dada yako tu akisimama unatapatapa hivyo, mwanasiasa lazima uwe na ngozi ngumu, uwe na uwezo wa kusikiliza wenzako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie Waheshimiwa Wabunge wa Chama cha Mapinduzi ukiona mtu anapiga kelele ujue tayari imemgusa huyo na sindano imeingia. Ndiyo maana Chama cha Mapinduzi, chama kikomavu, mnazungumza, tunawasikiliza na tunagusa vifungu.
Ni kwa sababu tumesimama hapa kutetea wanyonge, waandishi wa habari lakini wengine hapa wanachofanya ni kuwaonyesha waliowatuma kwamba nilizungumza. Sisi tunawawakilisha wananchi, wanyonge, tusimame na tuzungumze kwa niaba ya wanyonge, tuache kutumiwa na matajiri wachache wenye vyombo vya habari ambao wanataka kuendelea kukandamiza waandishi wa habari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naona yanatosha, yamewaingia, wameelewa na nina imani Serikali yangu yale inayohitaji kuyafanyia kazi yamechukuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ameniwezesha afya njema na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili na niweze kuichangia bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya kwa pamoja na Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Mwigulu Nchemba pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Olenasha kwa kazi nzuri waliyonayo katika kuiongoza Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi zangu, napenda nichangie katika maeneo yafuatayo:-
Eneo la kwanza ni eneo la kilimo, hususan zao la korosho. Ulianzishwa mfuko wa kuendeleza zao la korosho na madhumuni ya mfuko ule, pamoja na mambo mengine lakini pia kujenga viwanda vya korosho. Mfuko ulianza kwa kutuahidi kwamba tutaanza kujenga viwanda vitatu vya korosho, maeneo yakachaguliwa, lakini mpaka sasa hivi, imebaki ni hadithi, hatujui huo mfuko unapata shilingi ngapi na zinatumika vipi?
Kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri, huu mfuko ni lazima kwanza ukaguliwe na pia tuangalie, kwa sababu mara ya mwisho tumeoneshwa asilimia 41 tu ndiyo inayoenda katika kuendeleza zao la korosho. Kinachobaki kwa kweli hakieleweki, sana sana kinaenda kwenye utawala. Kwa hiyo, naomba uangalie sana katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kupunguza makato katika zao la korosho. Nimtahadharishe Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba kuna watu wamejipanga huko kuja kumwomba arejeshe baadhi ya makato.
Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba uendelee kuwa na msimamo wako huo huo, usibabaishwe wala usitetereshwe na baadhi ya watu wanaotaka kukuyumbisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni suala la uendeshaji wa minada, katika suala zima la Stakabadhi ya Mazao Ghalani. Huu mfumo ni mzuri sana na wananchi wanaupenda sana, tatizo uwazi hauko vizuri. Tumeelezwa katika kikao cha RCC kwamba korosho mwaka huu imenunuliwa mpaka shilingi 2,950 lakini kitu cha kushangaza, anakuja Afisa Ushirika anasimama anasema kwamba wanasiasa ndio wanaosumbua katika zao hili la korosho. Anasema kwamba sisi katika Wilaya yetu, koroshozimeuzwa kwa shilingi 2,060 tu. Sasa zile bei zinazotajwa kwenye RCC na ambazo wanatajiwa wananchi, kidogo kuna utata. Wakitafuta sifa, wanatutajia bei ya juu; wanapotaka kwenda kuwapa wananchi, wanashusha ile bei. Sasa tuelewe vipi?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa ufafanuzi, atuambie mwaka huu Korosho zimeuzwa kwa shilingi 2,950 au zimeuzwa kwa shilingi 2,060? Tupate ufafanuzi wa hilo ili wananchi wetu waweze kupata haki. Sasa hivi tunavyozungumza, Tandahimba vyama 149 wanadai zaidi ya shilingi bilioni 1.4 na hayo ni maelezo ya Mkuu wa Wilaya na Masasi pia wakulima wanadai pesa zao za korosho.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba wananchi wapate malipo yao. Wananchi wote wanaohudumiwa na MAMCU na TANEKU ambao wanadai malipo yao ya pili, walipwe ya mwaka huu na miaka mingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nilitaka kulichangia ni suala la wavuvi. Ukiangalia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri utakuta kuna pembejeo za wakulima na pia kuna pembejeo na jinsi ya kuendeleza wafugaji. Ukija kwa upande wa wavuvi, sana sana kuna mikakati ya kuzuia uvuvi haramu; hatukatai, lakini tungependekeza suala hilo liende sambamba na kuwawezesha wafugaji kwa vifaa; vitendea kazi. Wavuvi wetu wengi wanavua kwa kutumia zile zana za zamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka wakati Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, akiwa Waziri wa Uvuvi, kwa kweli alikuwa na mipango mizuri sana ya kuwawezesha wavuvi. Na mimi katika Wilaya yangu alikuja katika maeneo ya Msangamkuu, wakawawezesha wavuvi katika Kijiji kimoja tu, alitoa zaidi ya shilingi milioni 250. Sasa baada ya yeye kuhamishwa Wizara ile, mipango ile yote iliishia pale pale. Naomba Mheshimiwa Waziri Mwigulu Nchemba uangalie mipango ile, pamoja na kwamba ilikuwa inapitia MACEMP lakini ilisimamiwa na Waziri Mheshimiwa Dkt. Magufuli kipindi kile akiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Tunaomba wavuvi wawekewe mipango thabiti ya kuwaendeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba niongelee suala la wafugaji. Wafugaji wanahangaika kwa sababu wanatafuta malisho na maji kwa ajili ya mifugo yao. Tunaomba katika bajeti yako ioneshe mnajenga majosho mangapi na mnawatengea maeneo gani waende lakini pia wapatiwe maji, kwa sababu kitu kikubwa kinachowafanya wanahangaika wanaende kugombana na wakulima ni kutafuta maji na malisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba maeneo yatengwe ya wakulima yajulikane na ya wafugaji yajulikane, lakini ya wafugaji, tunaomba mwongeze kuwawekea majosho pamoja na maeneo ya kunyweshea mifugo yao, hapo ndipo mtakapoweza kuwafanya wafugaji wasihame eneo moja hadi lingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hii naomba wasiachiwe Halmashauri peke yao, Halmashauri wana majukumu mengi sana ya kutekeleza katika ngazi zao zile. Tuiombe Wizara mama ndiyo itoe mchango wa kuziwezesha Halmashauri kule chini ili ziweze kujenga majosho. Tukiwaachia Halmashauri peke yao kwamba watenge maeneo wao, wao wajenge majosho, kwa kweli tutakuwa tunawaonea.
Wizara itenge pesa kwa kushirikia na hizo Halmashauri ili kujenga majosho pia na kujenga maeneo ya kunyweshea hiyo mifugo. Napenda nimalizie kwa kuwashukuru sana wapiga kura wangu wa Jimbo wa Mtwara Vijijini kwa kuniamini kwa kipindi cha tatu, kuwa Mbunge wao. Napenda niwahakikishie kwamba sitawaangusha, nitafanya kazi na wao bega kwa bega, kwa maendeleo ya Jimbo letu la Mtwara Vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasisitiza tena suala la wavuvi kuwezeshwa, si suala tu la kwenda kuwakamata kuchoma nyavu zao na uvuvi haramu. Hakuna mtu anayependa kuvua kwa kutumia baruti, vijana wetu wanakufa; lakini wanafanya vile kwa sababu hawana mitaji, hawana zana za kuwawezesha kupata nyavu za kisasa, boti za kisasa na kupata injini za kuwawezesha kwenda kuvua katika kina kirefu. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atueleze, wavuvi ametutengea kiasi gani na za kufanyia nini? Maana yake siku zote tunasikia doria.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wavuvi na wenyewe wanatozwa tozo nyingi sana kwenye leseni; akitoka Mtwara anatozwa, akienda Kilwa anatozwa, akienda Msumbiji anatozwa. Tunaomba akilipia leseni, basi iwe ni hiyo hiyo, lakini kuna tozo nyingi sana; kila anachokwenda kukivua kule baharini kinatozwa. Kwa hiyo, nasema kabisa na lenyewe tuliangalie.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa upande wa wakulima wetu hasa wa zao la Korosho, tumesikia sasa hivi kuna suala commodity exchange, lakini sisi kama Wabunge hatujapata hata maelekezo, huo mfumo unaendaje ili tukawe wapambe wa kukusaidia mfumo huo kufanya kazi.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema na uzima na kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili nami niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza nimshukuru na kumpongeza Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kutuletea mwekezaji ambaye ana nia ya kujenga Kiwanda cha Sulphur kule Mtwara, namshukuru kwa hilo. Nampongeza kwa hotuba nzuri ambayo siyo tu imeandikwa vizuri, lakini pia amewasilishwa vizuri sana na kila mtu atakubaliana na hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema Serikali ya Awamu ya Tano ni ya viwanda na tunaunga mkono sana hilo. Ushauri wangu kwa Serikali yangu ni kuhakikisha tunatoa vikwazo vyote vile ambavyo wawekezaji wanakumbana navyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wangu wa Mtwara, naomba nianzie huko. Tunaye mwekezaji ambaye ameonesha nia ya kutaka kujenga Kiwanda cha Mbolea na tayari wenzetu wa EPZA wamemuonesha eneo la kujenga kiwanda tangu mwaka 2015 Aprili, lakini mpaka tunapozungumza sasa hivi, anashindwa kuanza kujenga kiwanda kwa sababu Wizara ya Nishati na Madini wameshindwa kumhakikishia upatikanaji wa gesi kwa zaidi ya miaka minne ijayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi wakati watu wa EPZA wanakuja kumuonesha eneo, walikuwa hawajazungumza na Wizara ya Nishati na Madini? Mwekezaji anaomba uhakika, kiwanda kile kitachukua zaidi ya miaka minne kukamilika, anaomba ahakikishiwe baada ya miaka minne kupewa gesi, mpaka leo Wizara ya Nishati na Madini haijampa uhakika kama watampa hiyo gesi. Kwa kweli kama Mwanamtwara, nasikitika sana, kwa sababu kiwanda hiki ni cha mfano. Mwekezaji alikuwa anafanya ubia na Halmashauri zote za Mkoa wa Mtwara na tayari tulishakubali, eneo wamepewa, lakini gesi hajapewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja, atueleze amefanya juhudi gani za kumsaidia mwekezaji huyo kupata gesi ili Kiwanda cha Mbolea ambapo nchi inaagiza mbolea kwa zaidi ya asilimia 90, lakini anakuja mwekezaji anataka kujenga hapa, tunamwekea vikwazo. Hivi tuelewe kuna lengo gani ambalo sisi wengine hatulifahamu? Haiwezekani gesi itoke Mtwara lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza hakuna kiwanda hata kimoja kimepewa gesi katika mkoa ule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo nataka kulichangia, ni suala la maeneo ya EPZA. Kama kweli tunahitaji kuwa na Serikali ya Viwanda, ushauri wangu ni kuiomba Serikali itafute fedha, ilipe fidia maeneo yote ambayo wanakusudia kuwa ni maeneo ya uwekezaji kwa maana EPZA na SES ili wawekezaji wanapokuja wasipate usumbufu wa aina yoyote wa kutafuta maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waziri atakapokuja atuambie, ana mikakati gani ya kuhakikisha kwamba maeneo ya EPZA yote yanalipiwa fidia kwa wakati ili yawe tayari, yasafishwe, yawekewe uzio tayari akija mwekezaji unamwonesha kwamba eneo la kuwekeza ni hili hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulianzisha ushuru wa korosho ambayo inasafirishwa ghafi kwenda nje, yaani export levy ili kuhakikisha kwamba, badala ya wafanyabiashara kupeleka korosho nje, wazibangue hapa. Lengo la ushuru ule ilikuwa ni kuwakatisha tamaa wale wanaopeleka korosho bila kuzibangua ili wawekeze viwanda katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitapenda Mheshimiwa Waziri atakapokuja atueleze tangu tumeanzisha export levy mpaka sasa hivi ni viwanda vingapi vimeweza kujengwa. Kama hakuna kiwanda chochote, ameshauri nini, kwamba kodi ile iongezwe kwa kiasi gani? Wasiwasi wangu ni kwamba, labda ile export levy ni ndogo kiasi kwamba hakuna sababu, mtu anaweza akalipa na bado akapeleka nje kuliko akizalisha korosho ndani ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulichangia ni suala la kulinda viwanda vyetu. Kama tumeamua kweli kuwa nchi ya viwanda, ni lazima suala hilo liende sambamba na ulindaji wa viwanda vyetu vya ndani. Tanzania tuna uwezo wa kujilisha au kujitosheleza sisi wenyewe kwa mafuta ya kula, tuna uwezo wa kuzalisha alizeti. Tunayo Mikoa kama Singida, Tabora, Dodoma na kanda nzima ya kusini huku, tuna uwezo wa kuzalisha alizeti na kuweza kuzalisha mafuta ya kujitosheleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote yatategemea iwapo tutakuwa tumeweka sheria ya kulinda viwanda vyetu. Kuna mafuta mengi sana ya kula yanatoka nje, wakisingizia kwamba mafuta hayo hayajakamilika, yaani yanakuja kusafishwa huku kwetu, lakini kimsingi yakifika hapa wanakuja tu kuya-park na kuanza kuyauza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Waziri wa Fedha pamoja na Waziri wa Viwanda na Uwekezaji, watuambie wana mikakati gani ya kulinda viwanda vyetu vya mafuta ya kula hapa nchini? Wenzetu Uganda wanafanya, Rwanda wanafanya, kwa nini sisi tuwe ni eneo ambalo mtu yeyote anayetaka kuleta mafuta ya aina yoyote ambayo hatuna hata uhakika wa usalama wa afya zetu, tunaruhusu watu kufanya hivyo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumsikia Mheshimiwa Waziri anatuambia katika upande wa viwanda vya mbolea na korosho kule Mtwara anatuletea viwanda vingapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, namwomba tu Mheshimiwa Waziri ajiandae kuja kuniambia kiwanda kile cha mbolea ana mikakati gani au anamwezeshaje yule ili aanze kujenga kile kiwanda?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenijalia afya na uzima na kuweza kupata nguvu ya kuweza kuwawakilisha wananchi wangu wa Jimbo Mtwara Vijijini na Mkoa wa Mtwara kwa ujumla na Watanzania.
Napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya kwa sababu Wizara hii ni zaidi ya Wizara tatu kama tulivyozoea kuziona, lakini nina imani kabisa kwamba ataweza kuzimudu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri, kile kitendawili chetu cha wananchi wa mkoa wa Mtwara kuhusu barabara yetu ya uchumi angalau mwaka huu tunaziona kilometa 50 zikiwa zimetengewa pesa. Ametuhakikishia kwamba kilometa hizo 50 kutoka Mtwara mpaka Mnivata ujenzi utaanza katika mwaka wa fedha 2016/2017. Mheshimiwa Waziri tunakushukuru sana kwa hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, isipokuwa ningependa tu kusisitiza, Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli wakati anaomba kura alituahidi akishinda zile kilometa 159 zinazobaki kutoka Mtwara - Newala - Masasi watagaiwa wakandarasi kilometa zote ili ujenzi uweze kukamilika kwa wakati. Mheshimiwa Waziri nitapenda wakati unatoa ufafanuzi utuelezee utaratibu uliopo kwa zile kilometa ambazo zimebaki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda pia nilizungumzie ni kuunganisha barabara zetu za mkoa na mkoa lakini pia kuunganisha nchi na nchi. Mheshimiwa Waziri tunazo barabra zetu zinazotuunganisha Mtwara na majirani zetu wa Msumbiji, kutoka Mtwara - Kilambo na kutoka Mtwara - Msimbati kimekuwa kilio cha muda mrefu, tumekuwa tukiomba zijengwe kwa kiwango cha lami kama ambavyo mipaka mingine yote inaungwanishwa. Kwa hiyo, nitataka kusikia ni lini mkoa wa Mtwara utaunganishwa na Msumbiji kupitia kivuko cha Kilambo na Msimbati kwa kujengwa kwa kiwango cha lami hasa ukizingatia kwamba Msimbati ndiko ambako gesi inatoka na tuna vitega uchumi vyetu vingi kule vya thamani ambavyo kwa kweli lazima tujenge barabara ya uhakika ambapo tutaweza tukaenda wakati wowote bila kujali mvua au jua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ni bandari. Katika bajeti ya mwaka 2015/2016 tuliambiwa kwamba majadiliano na wawekezaji upande wa Mtwara yamekamilika kwa ajili ya kujenga gati nne katika bandari ya Mtwara, leo Mheshimiwa Waziri anatuambia kwamba majadiliano yale ambayo tuliambiwa yamekamilika hayakufanikiwa na badala yake inataka kujengwa gati moja yenye mita 350, hatukatai sawa lakini lengo lilikuwa ni gati nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na utafiti wa gesi unaoendelea kule; zao letu la korosho na viwanda vingi ambavyo vinakwenda kule ikiwemo vya mbolea na hivyo vya kina Dangote kwa bandari iliyopo sasa hivi haitoshelezi na wakati mwingine inaleta usumbufu mkubwa sana hasa katika kusafirisha zao letu la korosho. Kwa hiyo, napenda Mheshimiwa Waziri atuambie gati zingine tatu zilizobaki mpango ukoje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunalo eneo la Kisiwa na Mgau ambapo eneo lingine tumempa Mheshimiwa Aliko Dangote ili ajenge bandari kwa ajili ya kusafirishia saruji na eneo lingine bandari yenyewe iliamua kuchukua kwa ajili ya kujenga bandari yake. Tathmini imeshafanyika, sasa hivi imebaki ni hadithi kesho, kesho kutwa. Amekuja Mheshimiwa Waziri Mkuu kule tuliambiwa baada ya siku tano fidia awamu ya pili italipwa. Lile eneo ambalo Dangote amepewa fidia ilishalipwa imekamilika, eneo ambalo bandari wamechukua kwa nini hamlipi? Dangote ameshalipa, wananchi wameshatumia pesa zao lakini wale ambao wanapaswa kulipwa na Mamlaka ya Bandari imebaki danadana. Sasa mnawagombanisha, kwa nini upande wa Dangote walipwe na upande wa bandari hamtaki kuwalipa?
Kwa hiyo, ningependa Mheshimiwa Waziri aje aseme ni lini watalipwa kwa sababu kila siku maelezo ni kwamba wanasubiri Bodi ya Bandari iundwe ili iweze kuridhia zile pesa kwa sababu pesa za kulipa fidia zipo shilingi bilioni 13, hiyo Bodi ya Bandari inaundwa lini ili mambo yaende? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulichangia ni kuhusu reli ya kutoka Mtwara - Songea - Mbamba Bay. Nimeona katika hotuba kwamba upembuzi yakinifu na usanifu umekamilika Februari 2016. Napenda kufahamu ujenzi wa reli hiyo ya kutoka Mtwara - Mbamba Bay na matawi yake ya kwenda Liganga na Mchuchuma utaanza lini? Kwa sababu uwekezaji unaofanyika kule Liganga na Mchuchuma, makaa ya mawe yaliyoko Ngaka bila kuwa na reli mradi ule Mheshimiwa Waziri itakuwa ni hadithi. Naomba Mheshimiwa Waziri aje atuambie ujenzi wa reli kutoka Mtwara - Mbamba Bay na matawi yake yanayokwenda Liganga na Mchuchuma utakamilika lini kwa Mtwara huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni ukarabati wa uwanja wa ndege wa Mtwara. Iliwekwa katika bajeti lakini mpaka sasa hivi hakuna fedha iliyotoka hata kidogo. Pia tuliambiwa uwanja ule utawekewa taa, mpaka sasa hivi taa hakuna. Tunachofanya pale ni kuazima taa za muda za wenzetu wa BG, hivi siku BG wakitukakatalia tunafanya nini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutonana na utafiti na uchimbaji wa gesi na mambo yanayoendelea kule Mtwara, kwa kweli ni lazima ule uwanja upate taa na ukarabatiwe. Uwanja ule ulijengwa mwaka 1965, hata mimi sijazaliwa na nimeshafikia mahali ambapo kama ni umri naweza nikasema zaidi ya nusu labda au nusu nimeshamaliza uwanja ule haujakarabatiwa. Tunaomba Mheshimiwa Waziri anapokuja aje atuambie uwanja unakarabatiwa lini na unawekewa taa lini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho, tunayo makampuni ya mitandao ya simu na kila mara wamekuwa wakidai kwamba wanalipa kodi ya huduma (service levy) katika Halmashauri, lakini Halmashauri zetu nyingi hazipati ushuru huu na badala yake unalipwa katika Halmashauri chache. Niiombe Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia taasisi zake ikusanye ushuru huu makao makuu na ugawanywe katika Halmashauri zote bila kujali ukubwa wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na mimi napenda niungane na wenzangu kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuichangia hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango kuhusu Hali ya Uchumi na Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2016/2017 pamoja na Makadirio na Mapato ya Matumizi kwa mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nianze kwa kumpongeza, kwa kuona umuhimu wa barabara yetu ambayo sisi wenyewe tunaiita ni barabara ya uchumi ya kutoka Mtwara kwenda Newala hadi Masasi, Mbinga hadi Mbamba Bay kuwa miongoni mwa miradi ya kipaumbele katika mwaka huu wa fedha. Mheshimiwa Waziri kwa hilo nakushukuru sana kwa sababu wananchi wa Mkoa wa Mtwara hasa barabara kutoka Mtwara - Nanyamba - Tandahimba, Newala - Masasi imekuwa ni kilio cha muda mrefu, hii ni barabara yetu ya uchumi inasafirisha korosho zaidi ya asilimia 80. Kila mwaka barabara hii inatengenezwa lakini ukiisha msimu wa korosho inaacha mahandaki. Kwa hiyo ikijengwa kwa kiwango cha lami kwa kiasi kikubwa itaboresha mazingira ya ufanyaji biashara ndani ya Mkoa wetu wa Mtwara, kwa hiyo nakushukuru sana kwa hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo nilitaka nilizungumzie ni suala la kupunguza ushuru wa korosho kwa wananchi. Napenda nilipongeze sana suala hilo kwa sababu siku nyingi tumekuwa tukilalamika wakulima wa zao la korosho wamekuwa wakikatwa makato mengi sana ambayo mengi hakuna hata moja linalowanufaisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kato la shilingi 10,000 kwa kila kilo eti kwa ajili ya kikosi kazi kufuatilia ununuzi wa korosho. Kikosi kazi hicho ni watumishi wa Serikali, viongozi wa Serikali ambao wamepewa majukumu ya kufanya kazi hizo. Kazi walizopangiwa ni pamoja na kusimamia ununuzi wa zao la korosho, lakini walianza na shilingi moja, ikaenda shilingi tano, ghafla ikaruka shilingi 10 kila kilo ya korosho wao wanataka walipwe kama viongozi kwa ajili tu ya kusimamia ununuzi wa zao la korosho.
Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu tulizonazo sasa hivi kwa mwaka tunazalisha zaidi ya tani 45,000, mwaka 2014 tulizalisha kwa mujibu wa korosho zilizosafirishwa nje ya nchi, tani 189,000. Mtwara peke yake inazalisha zaidi ya asilimia 80. Uchukue tu tani 100,000 zimetoka Mtwara na katika kila hizo tani 100,000 kila kilo moja mwananchi amekatwa shilingi 10 kwa ajili ya kuwalipa viongozi wanaosimamia ununuzi huo zaidi ya shilingi bilioni moja! Hivi tukienda kuwauliza hizo shilingi bilioni moja kwa biashara ya miezi mitatu wamezifanyia nini wataweza kutueleza? Wakati wana mishahara, wanatumia magari ya Serikali na kila kitu kimo wanafuatilia, mfano sasa hivi kuna utengenezaji wa madawati, wanalipwa shilingi bilioni moja kufuatilia utengenezaji wa madawati? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali na hasa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mkuu zao la korosho analijua hahitaji kuelekezwa na mtu, ana uzoefu alioupata kutokana na Chama chake cha Ushirika Kikuu cha Mkoa wa Lindi cha Ilulu na baada ya kuwa wamechoshwa na Ilulu wakaanzisha Lunali ambayo kwa kiasi kikubwa inafanya vizuri. Kwa hiyo, katika eneo hili Mheshimiwa Waziri Mkuu wala hahitaji kushauriwa na mtu, anajua mbichi na mbivu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu mimi pamoja na Wizara ya Fedha napongeza sana kwa yale makato ambayo yamepunguzwa na fedha hizi tunataka sasa ziende zikamnufaishe mwananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kule ndani eti kuna pesa zinakatwa kwa ajili ya unyaufu na korosho inaanza kunyauka baada ya miezi sita, lakini korosho zinafanywa minada kila wiki na ununuzi wa korosho unaanza mwezi wa kumi na unaisha kwa kuchelewa mwezi Januari. Sasa miezi hiyo mitatu hata kabla ya miezi sita kwa nini mwananchi akatwe eti ni unyaufu. Kwa hiyo niwaombe viongozi wenzangu wa Mtwara tumuunge mkono Mheshimiwa Waziri Mkuu, tuunge mkono Serikali yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wanakata shilingi 50 kila kilo ya korosho kwa ajili ya kusafirisha. Mimi katika Jimbo langu hakuna hata eneo moja ambalo linazidi zaidi ya kilometa 100, kwanza hazifiki. Sasa ndiyo kutaka kusema kwamba kila korosho inayosafirishwa tani 10 kutoka mahali popote, kilometa moja, kilometa mbili, kilometa tatu, tani kumi zinalipiwa shilingi 500,000. Kwa kweli huu ni unyonyaji wa hali ya juu, kwa hiyo, tumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nilitaka nilichangie ni ukusanyaji wa kodi za Halmashuri na TRA. Mimi sina ubishani wowote, property tax zikusanywe na TRA na vyanzo vingine vyote wakusanye lakini mchango wangu ni kwamba pesa zile zikishakusanywa, zote zirudi Halmashauri na zirudi kwa wakati kama ambavyo TRA inakusanya mapato yake kila mwezi ikishakusanya inayagawa katika Sekta mbalimbali ili ziweze kutumika katika mwezi unaokuja. Kwa hiyo, Halmashauri kila mwezi ipate mapato yake yaliyokusanywa katika mwezi ule ili yaweze kufanyiwa kazi katika Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunakusanya naomba pia tuwajengee uwezo watumishi wa Halmashauri ili zoezi hili liwe la mpito. Tufike mahali Halmashauri kupitia huu ugatuzi tunaozungumza wakusanye wenyewe. Isiwe kwamba mwaka huu waanze TRA halafu iwe ndiyo forever, tutakuwa hatuzijengei uwezo Halmashauri halafu ni kinyume cha sera yetu ya Ugatuzi wa Madaraka (Decentralization by Devolution). Kwa upande wa fedha huku tunaanza kurudi nyuma, lakini kama ni zoezi la mpito naliunga mkono lakini msisitizo wangu, kila mwezi Halmashauri zipelekewe pesa zao kwa sababu pesa hizi zimewekwa kwenye bajeti na wanazitegemea kwa ajili ya utekelezaji wa miradi.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo jingine ambalo ningependa nilichangie ni suala la mradi wa viwanda vya chuma Liganga na makaa ya mawe Mchuchuma. Miradi hii ni miradi ambayo ni kama viwanda mama ambavyo vyenyewe vitachochea viwanda vingine. Kwa hiyo, mchango wangu nilitaka niseme viwanda hivi pia viangalie na ujenzi wa reli ya kutoka Liganga na Mchuchuma kwenda Mtwara ambavyo vinaenda sambamba...
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga Naunga mkono hoja.
Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, nimesimama mbele yako kwanza, kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na kumshukuru Mwenyezi Mungu pia kwa kunipa afya kuweza kusimama na kuchangia katika mkataba huu.
Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kuanza kwa kumwomba Rais wangu kipenzi, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, asiusaini mkataba huu kwa manufaa ya Watanzania. Tunamwomba sana kama Wabunge, kwa sababu mkataba huu hauna manufaa hata kidogo kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sisi kutokusaini huu mkataba hatuwi wa kwanza na wala hatuwi kituko. Kwa upande wa SADC, Angola hawajasaini; kwa upande wa ECOWAS, Nigeria na Gambia hawajausaini mkataba huu. Kwa hiyo, sisi hatuwi wa kwanza kuukataa mkataba huu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mkataba huu hauna manufaa yoyote na Watanzania kwa sasabu zifuatazo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza, kwa mujibu wa takwimu za Benki Kuu, nchi kumi ambazo Tanzania tunafanya nazo biashara, nchi ambazo sisi tunachukua bidhaa, tuna-import kutoka kwao, ya kwanza ni Saudi Arabia; ya pili, ni China; ya tatu, ni India; ya nne, ni Falme za Kiarabu; ya tano, ni Afrika Kusini; ya sita, ni Uswiss; ya saba, ni Japan; ya nane, ni Marekani; ya tisa, ni Kenya; na ya kumi ni Andorra. Katika hizo nchi kumi, nchi za Ulaya ni Uswiss peke yake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ukienda kuangalia katika nchi ambazo sisi tunapeleka bidhaa zetu katika zile top five; ya kwanza ni China; ya pili ni India; ya tatu, ni South Africa; ya nne, ni Saudi Arabia; na ya tano, ni Kenya. Hakuna nchi yoyote ya Ulaya hapo.
Mheshimiwa Spika, pia ukiangalia katika FDI; ya kwanza ni Uingereza ambayo na yenyewe ni inajitoa kwenye Jumuiya ya Umoja wa Ulaya; ya pili, ambayo ndiyo itakuwa ya kwanza, kwa sababu Uingereza inatoka katika Jumuiya ya Ulaya, ni India; ya tatu ni Kenya; ya nne, ni Netherland; inafuata China, Marekani, Afrika Kusini, Canada, Ujerumani na Oman. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nchi zenyewe za Ulaya unaziona ni kama mbili tu. Kama tunataka kuua biashara zetu, kama tunataka kuua viwanda vyetu, tuingie katika huu mkataba. Wanachotaka hawa ni kutaka kuchepusha mfumo wetu wa biashara. Wanataka kututoa tusifanye biashara na Saudi Arabia, China na India; na kwa sasa hivi, masuala ya biashara wanaotawala duniani ni China, India na Marekani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hawa Jumuiya ya Ulaya wanataka kuturudisha tena tulikotoka. Wanataka tena scramble for Africa, hatuko tayari. Pia wanachokifanya Jumuiya ya Ulaya, kwa sababu makubaliano ya EPA ni kusaini Jumuiya ya Afrika kama nchi moja na sio mmoja, mmoja. Kwa hiyo, wanachotaka ni kuvunja Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki. Tuwaambie kabisa, Jumuiya ya Ulaya kwa kuanza kusaini na nchi moja moja badala ya kanda nzima kama Afrika Mashariki, wanataka kubeba dhima ya kuuwa Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, narudia tena, namwomba Mheshimiwa Rais, kwa kweli asisaini mkataba huu. Kuna mtu amesimama hapa akasema tusomewe mazuri yaliyoko katika mkataba. Mkataba tumekabidhiwa, angeusoma huu mkataba akatueleza yeye mazuri. Yeye anasimama, anasema tusaini, lakini hajasema hata moja zuri, anakusudia nini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, napenda nimuunge mkono Mheshimiwa Bobali aliyesema hivi sisi, tuna kitu gani tunachoweza kwenda kuuza Ulaya? Sana sana sisi tunategemea malighafi; tunategemea kuuza nyama, samaki, lakini je, tuko tayari? Tunao uwezo wa kushindana na bidhaa kutoka Ulaya au sisi tunataka kufanywa soko la kuja kutupa bidhaa zao za kuja hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nchi za Caribbean ambazo zilijiunga, tafiti zinaonesha zimepoteza mapato yao kuanzia mwaka 2009 hadi 2013, wamepoteza zaidi ya Euro milioni 74.
Mheshimiwa Spika, narudia tena, tusisaini mkataba huu, hao wanaoshabikia, ndio wafadhili wao. Sisi hatuko tayari kusaini mkataba ambao pia katika kifungu cha 96 cha Cotonou ambacho kinaoanisha na Ibara ya 136 ya EPA pia haki za binadamu zimo, ambamo ushoga umo. Tuko tayari sisi kuingizwa kwenye ushoga kwa kupitia hii biashara? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, narudia tena kusema siungi mkono hoja. Mkataba huu Mheshimiwa Rais tunakuomba usiusaini.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nashukuru kwa kunipa nafasi.
Kwanza nianze kwa kutoa pole kwa Wana-CCM wenzetu ambao walipata ajali na kupoteza
maisha kule Mkoa wa Kilimanjaro. Tunamuomba Mwenyezi Mungu aweke roho zao mahali
pema peponi na pia awape moyo wa subira familia zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo napenda niende haraka haraka
katika kuchangia hoja. Suala la kwanza nilitaka kumuuliza Waziri wa Miundombinu, hivi zile
Bombadier Mtwara zitaenda lini? Mimi nimezipanda kwenda Tabora, nimepanda kuja Dodoma,
kwa kweli ni ndege nzuri zinaenda kwa kasi, zinachukua muda mfupi sana. Mtwara ni miongoni
mwa viwanja bora sana ambavyo vimejengwa muda mrefu, kwa nini na sisi tunyimwe hiyo haki
ya kupelekewa Bombadier? Kwa hiyo, nilikuwa naomba atueleze lini hizo Bombadier zitaanza
kwenda Mtwara.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nililotaka kulizungumzia ni kuhusu barabara ya
kutoka Mbwenkulu kwenda Nangurukuru. Kwa kweli ile barabara kile kipande kimechakaa,
kinatitia na kinasababisha ajali nyingi sana. Ukitoka Somanga kwenda Daraja la Mkapa kile
kipande ambacho kimejengwa na Caraf unaweza mpaka kuandika hata barua, yaani huwezi
kujua kama uko kwenye gari. Tunaomba na eneo lile la kutoka Mbwenkulu kwenda
Nangurukuru nalo lirejewe na liwe na ubora ule ule unaofanana kutoka Somanga kwenda
Darajani. Huwezi kuamini kama uko ndani ya gari. Tunaomba kwa kweli lile eneo lirudiwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nilitaka nilizungumzie ni kuhusu umeme.
Katika Mji wa Mtwara juzi nimepokea message kwamba wanaomba samahani kwamba siku hizi
kuanzia saa moja mpaka saa nne usiku hakuna umeme. Sasa hivi anaeanza kupata umeme
kuanzia saa tano huo kweli si afadhali hata tungekuwa tunapewa saa moja mpaka saa nne?
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachosababisha ni kwamba zile megawati 18 zimeshakwisha
sasa hivi, kwa hiyo ikitokea shoti kidogo kwenye jenereta moja ni tatizo. Tunaomba yaongezwe
majenereta hali ni mbaya katika Miji ya Mtwara na Lindi. Tunaomba Wizara ya Nisahati ije na
kauli inaongeza lini megawati lakini hata ile mitambo iliyopo wanaifanyia lini matengenezo ya
uhakiki? Huwezi kuwa na mahitaji megawati 18 na zilizopo megawati 18. Kwa kweli hapana,
tunaomba hilo waliangalie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na suala lingine ambalo nilitaka nilizungumzie ni suala la
barabara kutoka Mtwara kwenda Newala - Masasi ni kilometa 30, tunataka kujua mkataba
unasainiwa lini Mheshimiwa Waziri? Mheshimiwa Rais alituambia akiingia madarakani kazi ya
kutoka Mtwara Mnivate inaanza na eneo lililobaki ataweka wakandarasi wanne ili wajenge kwa
wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba vile viatu vya Mheshimiwa Rais, ambaye alikuwa
Waziri wa Ujenzi aliyekutangulia ujitahidi ili viweze kukuenea.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti nikushukuru kwa kunipa nafasi nichangie taarifa yetu ya Kamati ya Bajeti. Kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kuongeza bajeti ya Serikali kwa upande wa miradi ya maendeleo hadi kufikia asilimia 40. Tunachoomba tu kwamba pesa ziendele kwenda kwa wakati ili miradi itekelezwe kama ambavyo tumepanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia niipongeze Serikali kwa hatua ya kusaini mkataba kwa ajili ya ujenzi wa reli ya kati. Reli ya kati ni kama mishipa ya fahamu ya mwili wa binadamu kwa uchumi ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuendelea kwa kutegemea bidhaa na malighafi zetu kubebwa na Lori moja moja kutoka Dar es Salaam mpaka Kigoma, Mwanza na kwenda nchi za jirani na hilo hilo lirudi lije lichukue kwa kweli hili haliwezi kutufikisha mbali lakini kwa hatua hii ya Serikali kusaini Mkataba wa kujenga reli tena kwa standard gauge kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro kama hatua ya kwanza naipongeza sana na tunaomba vipande vilivyobaki basi vifanyiwe haraka ili mradi huo uweze kukamilika kwa wakati ili kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa Serikali kulisisitizia ni eneno la EPZA. Kamati ilitembelea eneo la Mheshimiwa Benjamin Mkapa pale Mabibo, kwa kweli kule ndani kuna kazi nzuri sana inayofanyika na kuna ajira nyingi sana zinazotolewa kwa vijana wetu. Bidhaa zinazozalishwa pale ni za ubora wa hali ya juu na za mauzo ya nje ambazo zinatuingizia pesa za Kigeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kitu kama kile tulitegemea Dar es Salaam pale tuwe na EPZA kama mbili na ikiwezekana angalau kila mkoa tuwe na eneo la EPZA kwa sababu ni eneo ambalo linakuza ajira, linaingiza mitaji, linatuongezea teknolojia kutoka nje. Eneo la Kurasini tayari Serikali ilishalipia fidia kwa hiyo, tunaomba wawezeshwe EPZA kuweza kujenga miundombinu na hivyo kuwavutia wawekezaji kuja kuwekeza katika eneno la EPZA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu, kwa sababu umenipa dakika tano, ningependa kusisitiza suala la utekelezaji wa mradi wa Mchuchuma na Liganga. Mradi huu umezungumzwa kwa muda mrefu sana na ni mradi ambao kwa kweli utaleta viwanda mama, viwanda vya vyuma, viwanda ambavyo vitaleta viwanda vingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua iliyofikiwa si mbaya kwa maana kwa upande wa uzalishaji wa umeme kwa kutumia makaa ya mawe sawa, lakini upande wa chuma. Makaa ya Mawe yale na chuma tunategemea kwa kiasi kikubwa yasafirishwe kupitia Bandari ya Mtwara na reli ambayo tayari feasibility study ilishakamilika, upembuzi yakinifu ulishakamilika sasa hii tathmini ya fidia ilishakamilika, kwa hiyo, tunaomba fidia ile iweze kulipwa na ile reli kutoka Mtwara kwenda Mchuchuma na Liganga na matawi yake kwenda Mbamba Bay upewe umuhimu wa hali ya juu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu chuma kile bila reli ile na makaa ya mawe yale bila reli ile kwa kweli hatuna barabara za kuweza mzigo mzito kama ule sana sana barabara zetu zitakuwa ni za kujenga baada ya miaka miwili zimeharibika halafu tunawalaumu waliojenga au waliosimamia kuzijenga lakini ni kutokana na mzigo mzito kwa hiyo nisisitize mradi wa Liganga na Mchuchuma na pia reli ya kutoka Mtwara, Liganga na Mchuchuma vitekelezwe kwa wakati muafaka ili kukuza uchumi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana ulinipa dakika tano nisingependa unigongee kengele, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake pamoja na wataalam wao kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kutekeleza majukumu yao. Nipongeze Serikali kwa kuanza kujenga reli kwa kiwango cha SGR, pia nimpongeze Waziri kwa kazi ya ujenzi na upanuzi wa barabara ya Mtwara. Naomba Serikali kuona umuhimu wa kukarabati uwanja wa ndege wa Mtwara kwani umechakaa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kuiomba Serikali kuhusu kuharakisha na kuongeza kiwango cha pesa kwa barabara ya Mtwara, Newala, Masasi kwa mujibu wa mkataba. Serikali pia ianze ujenzi wa reli ya Mtwara - Mchuchuma na Liganga Mbamba bay. Reli hii ni muhimu sana kwa uendeshaji wa bandari ya Mtwara.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu Afya na Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii pamoja na wataalam wao kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru Waziri kwa kukipatia gari kituo cha afya cha Kitere, suala ambalo nina imani litasaidia sana katika kuboresha huduma za rufaa kwa wagonjwa hasa akina mama na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Waziri kuongeza watumishi wa afya katika vituo vya afya vya Nanguruwe, Kitere na Mahurunga ili viweze kutoa huduma bora kwani vituo hivyo vinavyo vifaa vya kisasa vya kutolea tiba, lakini baadhi yake vinashindwa kutumika kutokana na uchache wa wataalam wenye weledi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali pia kuongeza udahili wa wauguzi, maafisa tabibu, wafamasia na wataalamu wa maabara na kufadhili masomo yao ili tuweze kuwapa masharti ya kwenda kufanya kazi katika maeneo yenye upungufu kwa muda maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali kuonesha nia ya dhati katika ujenzi wa hospitali ya Kanda ya Kusini. Kwa Kusini Mkoa wa Lindi na Mtwara ni kanda pekee isiyokuwa na Hospitali ya Rufaa ya Kanda na kwa miaka miwili mfululizo kiasi kinachotengwa kwa hospitali hiyo kwanza ni kidogo na pili, fedha hizo hazitolewi. Kwa kifupi ni kama ujenzi umesimama, Mheshimiwa Waziri iwapo hutatoa mikakati inayotia moyo na yenye kuonesha nia ya kukamilisha ujenzi wa hospitali hii nakusudia kuondoa shilingi kwenye mshahara wa Waziri na kwenye bajeti ya Wizara.

Mheshimi Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika taarifa za Kamati hizi mbili. Pia nichukue fursa hii kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati kwa kazi nzuri waliyoifanya kwa ajili ya kuishauri Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa kwanza wa miaka mitano wa maendeleo ulikuwa na lengo la kutoa vikwazo vya kimaendeleo ambavyo vilikuwepo kipindi kile ikiwa ni pamoja kuongeza upatikanaji wa umeme, kuboresha miundombinu ikiwa ni pamoja na ujenzi wa reli na barabara pamoja ya kuboresha bandari zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango wa Pili ambao tunao ambao una lengo la kuhakikisha kwamba tunakuwa na uchumi wa viwanda. Naliunga mkono sana hilo lakini wasiwasi wangu nahisi tunaweza tusifike mbali kwa sababu bado vile vikwazo ambavyo vilikuwepo katika mpango wa kwanza vinaelekea kwamba bado tunaendelea kuwa navyo na vingine si kwamba vikwazo halisi vipo lakini baadhi tu ya watu wanaamua kuvifanya viwe vikwazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Waziri wa Viwanda na Biashara, vile viwanda wanavyosema anatembea navyo mfukoni kwangu kwa kweli amenisaidia sana na tumefikia hatua nzuri. Nilimwomba kiwanda kwa ajili ya sulphur kwa sababu sisi kule ni wakulima wa korosho na sulphur kwa kiasi kikubwa tunaagiza kutoka nje, basi tuliomba angalau hata kufunga waje waifungie kule kwetu lakini pia tunaweza kutengeneza kwa sababu tunayo gesi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari mwekezaji amekuja, Mtwara amekwenda, ardhi tumempatia sasa hivi yuko hatua za mwisho na nina imani kabisa huko TIC atamaliza lakini wasiwasi wangu ni upande wa nishati, upande wa upatikanaji wa gesi na upande wa umeme, ndiyo maana nikasema kwamba vile vikwazo bado vipo. Gesi inatoka Mtwara lakini mpaka tunapozungumza hapa tunavyo viwanda zaidi ya viwili, vingine vinashindwa kujengwa; bado Wizara haina nia ya dhati ya kusaidia wawekezaji kuwapatia gesi au kuwapatia umeme wale ambao wanataka kuwekeza Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu; mwakani tutakapokuwa tunajadili Kamati ya Viwanda na Biashara iunganishwe na Nishati na Madini kwa sababu tulikotoka tulikuwa na changamoto sana ya ardhi kwa wawekezaji wetu kwenye viwanda. Sasa hivi hatuna tatizo kwenye ardhi, hatuna tatizo na Wizara ya Viwanda na Biashara, tatizo kubwa lililopo ni upande wa Wizara ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara tunavyozungumza sasa hivi umeme ni wa shida, mitambo inakufa kila mara, megawati 18 zinazozalishwa mahitaji zimeshazidi megawati 18 na hatuoni mipango ya uhakika ya kuhakikisha tatizo hilo linakufa. Tunacho kiwanda cha mbolea, tayari wamekuja Wizara ya Viwanda na Biashara imewasaidia imetoa eneo lake la EPZA, Wizara ya Miundombinu wamejenga barabara ya lami mpaka katika hilo eneo, lakini mpaka sasa hivi watu wa Wizara ya Nishati hawajaonesha nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba kiwanda kile kinakuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndani ya Serikali kwa mtazamo wangu, wenyewe kwa wenyewe wanakwamishana na kwa kiasi kikubwa nahisi hata vile viwanda tunavyovihisi kwamba viko mfukoni si ajabu vinakwama kwenye nishati. Kwa hiyo, tuseme bila kigugumizi kwamba Wizara ya Nishati isaidie Wizara nyingine katika kuhakikisha kwamba viwanda, kama uchumi wetu ni wa viwanda, nishati kwa kiasi kikubwa itatumika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiingii akilini kwamba Mtwara ile mpaka sasa hivi hawajamuingizia umeme hata mtu mmoja, hawajamuingizia gesi hata mtu mmoja na wala hawana mpango. Pia nimuombe Waziri wa Viwanda na Biashara atuelezee mpango mkakati wa kuendeleza viwanda katika Mji wa Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo ardhi, eneo la EPZA, wengine wanalia fidia sisi fidia ilishatolewa tangu mwaka 2000, eneo lipo kuzunguka bandari, hakuna matatizo ya fidia wala nini, wanasubiriwa wawekezaji. Eneo ambalo Dangote amejenga kiwanda ni hekta 17,000, yeye amepewa 4,000 tu nyingine zipo za kumwaga hazihitaji fidia, hazihitaji kitu chochote, Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara atuelezee na Waziri wa Nishati na Madini mikakati yao ya kuhakikisha gesi inatumika katika viwanda katika Mji wa Mtwara. Ni haki yetu watu wa Mtwara na sisi kupata maendeleo ya nchi hii na wala hatuombi favour. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ninalotaka nizungumzie, kama nilivyotangulia kusema eneo la EPZA Mtwara tunalo fidia ilishalipwa tangu kipindi cha Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, eneo lipo wazi. Sambamba na EPZA ya Mtwara, tunayo Kurasini, tunayo pale Benjamin Mkapa na katika mikoa maeneo mbalimbali, EPZA ndiyo njia rahisi kama walivyotangulia kusema, ya kuhakikisha nchi inaendelea kwa haraka. Watu wanakuja na mitaji yao, wanakuja na teknolojia yao, sisi tunachopata pale, kwanza tunapata ajira, tunapata teknolojia mpya na pia tunapata pesa za kigeni. Hivi kwa nini tusihakikishe kwamba hii EPZA inakwenda kwa kasi, hata China tunaosema wameendelea walianzia na EPZA, kule akina Shenzhen, maeneo mengi, akina Guangzhou, kote walianza kama EPZA, kwa nini tusiige hayo mambo mazuri na sisi tukaweza kunufaika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wale wanaosema kwamba viwanda vile ambavyo vilibinafsishwa vihakikishe vinafanya kazi iliyokusudiwa. Kule kwetu Mtwara viwanda vya korosho watu walipewa kwa bei ya kutupa lakini hakuna hata mtu mmoja anayebangua korosho, wengi kazi yao wamefanya maghala wanayakodisha kipindi cha ununuzi wa korosho wanaona inawalipa kuliko kufanya viwanda, korosho zetu zinakwenda nje zikiwa hazijabanguliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kuhakikisha kwamba viwanda vile kama watu madhumuni waliyopewa, kwa sababu hawakupewa kwa bei ya soko, walipewa kwa bei ya kutupa, wahakikishe aidha, wafanye kazi iliyokusudiwa au wanyang‟anywe wapewe watu wengine ili waweze kufanya kazi iliyokusudiwa. Haiwezekani kiwanda cha korosho leo kinageuzwa ghala la kuhifadhia korosho, kwa kweli hilo tulisimamie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Waziri wa Viwanda na Biashara, anahangaika katika kutafuta viwanda. Sisi kama Wabunge katika maeneo yetu lazima na sisi tumuunge mkono, amenipa mwekezaji nimekwenda naye nimemtembeza katika maeneo yote ya ardhi na akachagua eneo analolipenda na tumefikia hatua nzuri, nina uhakika kile kiwanda kitafika, lakini wasiwasi wangu Wizara ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wa Ardhi kwa sababu ili uweze kuwekeza vitu vikubwa muhimu ni ardhi, nishati na wenzetu hao Wizara ya Viwanda na Biashara ambao tunategemea waweke mazingira mazuri. Kwa sababu hawezi kujenga viwanda Waziri wa Viwanda na Biashara. Kazi ya Waziri wa Viwanda na Biashara ni kuweka mazingira mazuri ambayo anayaweka, Waziri wa Ardhi hana matatizo kwenye uwekezaji, ardhi, migogoro anatusaidia kutatua, lakini Nishati na Madini kwa kweli kama tunataka tuwe na uchumi wa viwanda Wizara ya Nishati na Madini kwa kweli iamke. Ndiyo tunapata umeme wa REA vijijini, lakini ule ni kuwasha tu vikoroboi badala ya vikoroboi sasa tunaleta bulb, tunahitaji umeme uzalishe, uinue uchumi wa nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami ningependa kuchangia hoja. Niwapongeze watoa hoja wote na hivyo nianze kwa kuunga mkono hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza ningependa kuzungumzia suala la elimu na hasa masuala mazima ya ufaulu. Katika wilaya nyingi na mikoa mingi ambapo matokeo ya kidato cha pili na kidato cha nne yamekuwa siyo ya kuridhisha, asilimia kubwa uamuzi au hatua zilizochukuliwa ni kushusha vyeo walimu wakuu au wakuu wa shule. Mimi sidhani kama mwalimu peke yake anaweza akawa ndiyo sababu ya shule kufeli au kufaulu. Mimi napenda nishauri katika zile Wilaya ambazo kila mtihani uliofanywa zimekuwa za mwisho hebu tufanye utafiti wa kina tujue kwa nini wilaya hizo zimefanya vibaya. Haiwezekani kwenye Mkoa wangu Wilaya moja hiyo hiyo matokeo ya kidato cha nne wa mwisho, matokeo ya darasa la saba ya mwisho halafu tuone hatua ya kuchukua ni kushusha vyeo tu walimu, sidhani! Naomba tufanye tathmini ya kina ili tujue tatizo tuweze kuwasaidia na zile Wilaya na zenyewe zifanye vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye sekta ya afya na nianze kuzungumzia suala la uchache wa watumishi katika sekta ya afya. Kwa kweli hali ni mbaya, ukienda katika vituo vyetu vingi vya afya, hospitali majengo ni yanaridhisha, unakuta hospitali zetu sasa hivi nyingi ni safi, madaktari wanajitahidi hata wauguzi, kauli zinaridhisha lakini uchache wao unawaangusha. Katika baadhi ya Wilaya tunashindwa kutoa baadhi ya huduma kama upasuaji, kufungua baadhi ya zahanati, kwa sababu ya uchache wa watumishi. Niombe Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, wakati tukiendelea na uhakiki basi kama tulivyofanya kwa sekta ya elimu na sekta ya afya nayo tuiangalie, hali ni mbaya hasa katika Mkoa wangu wa Mtwara ambao ninaufahamu. Nina vituo vyangu vya afya ambavyo vimeshindwa kuanza huduma za upasuaji kwa sababu hatuna watumishi wa kuweza kutoa huduma hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la vifo vya akina mama limezungumziwa sana hasa kutokana na changamoto za uzazi. Mojawapo ikiwa kuzalishwa na watumishi ambao kwa kweli hawana utaalamu. Niombe hivi vituo vya afya, mlishaanza kuvifanyia tathmini na kuvipa madaraja, zoezi hili likamilike nchi nzima ili vile vituo ambavyo havina uwezo wa kuzalisha akina mama waambiwe kwamba siku zako zikifika pale huwezi kusaidiwa, wajue ili ajiandae, ikiwezekana aende akakae karibu na eneo ambalo ataweza kusaidiwa. Kwa sababu kama atahitaji damu wakati wa kujifungua, kama atahitaji operation wakati wa kujifungua ndiyo kusema kama atakuwa eneo ambapo hakuna huduma hizi huyo mama ndiyo tumeshampa cheti cha kifo.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka kulichangia ni tafiti zinaonesha maeneo ambayo wanaume wanafanyiwa tohara maambukizi ya UKIMWI yako chini sana kuliko maeneo ambayo hayafanyiwi tohara ambapo maambukizi ya UKIMWI yako juu sana, na hivyo hivyo maeneo ambayo tohara haifanyiki maambukizi ya kansa ya shingo ya kizazi pia yako juu. Niiombe Wizara ya Afya hili suala la tohara kwa wanaume lisiwe la hiari liwe la lazima. Kwa sababu kama tafiti zote zinatuambia maeneo mengine wanaume ambao hawajatahiriwa maambukuzi wako zaidi ya asilimia 21 kuliko wale ambao wametahiriwa. Kwa nini tusiseme ni lazima? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba, ile Mikoa ambayo wanatahiriwa, lile tendo wasiite suna, maana yake mtu anasema anakwenda kutahiriwa unaita suna, kitu kama ni suna maana yake siyo lazima, niwaombe kwa wale wanaotahiriwa tuseme faradhi ili kila mtu ahamasike. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana wote tulikuwa Morena, tumeambiwa haya, siyo kama nimeyatoa kichwani, ni taarifa zilizotolewa na Shirika la Afya Duniani, Wizara ya Afya wanazo. Tupeleke taarifa sahihi, kuhusu suala la tohara kwa wanaume. Tutawanusuru akina mama wetu tutapunguza maambukizi ya virusi vya UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Wizara ya Afya, tunazo hospitali zetu za Kanda, Kanda ya Kaskazini tunayo KCMC, Kanda ya Magharibi au ya Ziwa tunayo Bugando na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini tunayo Hospitali ya kule Mbeya, Kanda ya Kusini peke yake ndiyo imebaki ambayo haina Hospitali ya Rufaa ya Kanda, ujenzi umeanza lakini ni wa kusuasua. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, tusaidie katika hilo, gharama ya kumsaidia mgonjwa mmoja kuja hospitali kutibiwa kwa kumsafirisha kwa ndege kutoka Mtwara, Precision Air inafika mpaka shilingi milioni 12. Mimi mwenyewe nimesafirisha kijana ambaye alipata ajali ya gari kwa shilingi milioni nane kwa ATC, kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam, ni wangapi wanaweza gharama hizo? Kwa hiyo, tuwaombe wenzetu wa Wizara ya Afya mkamilishe ujenzi wa Hospitali ya Kanda ya Kusini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo Hospitali za Rufaa za Mikoa, naomba tuzifanye ziwe kweli Hospitali za Rufaa za Mikoa. Unakwenda Hospitali ya Rufaa ya Mkoa unakuta ina oxygen machine moja, wakija wagonjwa wawili mmoja anakuwa kwenye mashine mwingine hata kama anahitaji ile huduma hawezi kupata. Tuombe muweke MRI, muweke CT Scan, X-ray machines, angalau hata kwa Kanda. Kwa sababu tunazungumzia suala la ugonjwa wa kansa ya kizazi ndiyo ugonjwa ambao unaua sana akina mama, lakini huduma hiyo inapatikana hospitali ya Ocean Road peke yake, na ugonjwa huo mgonjwa akiwahi unatibika. Kwa hiyo, niombe basi huduma hii ipelekwe angalau kwenye Kanda. Hivi ni wangapi wenye uwezo, unatoka Rukwa, unatoka Kagera kwenda Dar es Salaam na kila dozi inapokuja uende, kwa kweli, ndiyo kule utatibiwa bure, lakini mara nyingi gharama za kwenda kule huwa wanajigharamia. Kwa hiyo niombe kwa kweli hili lifanyiwe kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la kuweka vifaa MRI, CT Scan na X ray machines siyo lazima Serikali ifanye, tunaelewa kwamba Serikali haina uwezo wa kugharamia kila kitu na tunaona unapokwenda kwenye hospitali pale Muhimbili kama mashine haifanyi kazi unaambiwa ukapime nje, kwa nini msiingie ubia mkafanya PPP, hizo mashine wakaja kuziweka kwenye hospitali zetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Wizara ya Afya mshirikiane muingie ubia, vitu kama MRI, CT Scan, X-Ray, kila baada ya miaka mitano teknolojia inabadilika na hatuwezi kwenda na kasi hiyo, lakini akiweka mtu binafsi ikipita muda wake unamwambia hamisha leta nyingine inayoendana na teknolojia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na timu yake yote kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika Wizara hii, pamoja na ukubwa na majukumu mengi lakini wanaonekana kuweza kuyamudu na kuimudu Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza napenda nipongeze kazi ya upanuzi wa Bandari ya Mtwara ambao tayari umekwishaanza. Ni imani yangu kwamba upanuzi ule wa bandari utasaidia sana katika kuharakisha maendeleo ya Mkoa wa Mtwara, Lindi na Ruvuma hasa ukizingatia kwamba sisi ni wakulima wakubwa wa korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupanua bandari ile sasa hivi hakutakuwa na sababu hata kilo moja kusafirishiwa mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam hasa inayozalishwa katika Mikoa ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la Liganga na Mchuchuma kwamba kule kuna uzalishaji wa makaa ya mawe, kuna chuma, tuna kiwanda kikubwa sana cha Dangote ambacho kinategemea hiyo bandari pia tunategemea chuma itakayozalishwa kule, makaa ya mawe na yenyewe pia yasafirishwe kupitia Bandari ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri suala la upanuzi wa Bandari ya Mtwara basi liende sambamba na ujenzi wa reli kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay na Liganga na Mchuchuma. Suala la upembuzi yakinifu limekamilika, tathmini ya mimea pamoja na nyumba maeneo ambapo reli itapita imeshakamilika. Kwa hiyo, namwomba sana suala hilo nalo liende pamoja ili ile bandari isije ikaleta mzigo mkubwa ukalazimika tena kusafiri kwa magari ambao utaharibu barabara ambayo kwa kweli tumekaa muda mrefu sana baina ya Mtwara na Ruvuma hatujawa na barabara ya kueleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine napenda kumpongeza sana Waziri na Serikali pamoja na Mheshimiwa Rais kwa kuanza kujenga reli ya kati. Reli ya kati ni sawa na mifumo ya damu au mifumo ya fahamu ndani ya mwili wa binadamu, reli hiyo ndiyo itakayoifanya bandari ya Dar es Salaam iweze kufanya kazi yake vizuri. Kwa hiyo, namwomba tu waharakishe hicho kipande cha kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro ambayo ni reli ya kisasa sana. Vipande vinavyobaki basi watangaze kwa haraka ili ujenzi huo ikiwezekana uweze kukamilika kwa muda mfupi sana, kwa sababu huo ndiyo ukombozi wa nchi yetu na maendeleo yetu kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine napongeza pia ndege ya Bombardier kuanza kutua Mtwara na Songea. Tarehe 30 imeenda kwa mara ya kwanza, nimeambiwa kwamba kutakuwa na ratiba nzuri tu zinazoeleweka. Ushauri wangu naomba ile ndege ya kwenda Mtwara inaunganisha pamoja na Ruvuma, unatoka Mtwara unaenda Ruvuma saa nzima, unatoka Ruvuma kwenda Mtwara dakika hamsini karibu na tano, halafu ndiyo utoke pale kwenda Dar es Salaam karibu tena dakika 50. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba route ya Ruvuma ikiwezekana iwe ni ya Ruvuma peke yake ili mtu akitoka Dar es Salaam anafika Ruvuma na akitoka Ruvuma anafika Dar es Salaam. Kutoka Mtwara mpaka ufike Ruvuma upite tena Mtwara kwa kweli inachukua muda mrefu sana na kama shirika kweli linataka kushindana na mashirika mengine ambayo yanaenda Mtwara hapo hamtaweza kushindana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu ni kwamba route ya Mtwara iunganishwe na ya Comoro kwa sababu kutoka Mtwara kwenda Comoro ni saa moja na kutoka Comoro kwenda Mtwara ni dakika kama 25 au nusu saa. Kwa hiyo, hapo utaweza ushindani. Huo ndiyo ushauri wangu kwamba hiyo route ya Dar es Salaam – Ruvuma – Mtwara waiangalie tena ikiwezekana Mtwara iambatanishwe na ya Comoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nilichangie ni suala la barabara ya kutoka Mtwara – Newala kwenda Masasi. Niishukuru Serikali kazi inaonekana kwamba inakaribia kuanza, Mkandarasi amepatikana na ameshaanza kukusanya vifaa tuna imani muda wowote ataanza ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika bajeti iliyotengwa mwaka huu ambao tunaenda nayo ni bilioni 21 na bajeti ambayo ipo sasa hivi ni bilioni saba. Kwa mujibu wa mkataba ule ni zaidi ya bilioni 90 na mkataba ni wa miaka miwili, sasa kwa pamoja tumetenga kwa miaka miwili bilioni 29, mkataba unataka bilioni karibu 90 na kitu. Sasa huyo Mkandarasi atajenga kwa fedha zipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iangalie hilo, vinginevyo tutakuwa tunamfanya Mkandarasi anakuwa site anaondoka. Mheshimiwa Waziri tunashukuru kwa sababu lazima ushukuru kidogo ulichokipata, tunashukuru kwamba sasa hivi ile ndoto imeanza kutimia, lakini pia iangaliwe bajeti ili barabara ijengwe kwa ubora unaokusudiwa, kwa sababu kama pesa zitakuwepo mkandarasi hana kazi ya kuondoka site na kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni suala la Uwanja wa Ndege wa Mtwara. Uwanja ule umejengwa kabla sijaanza hata darasa la kwanza na hata sijui umejengwa lini kwa sababu nimepata akili nimeukuta ule uwanja upo tayari. Tangu kipindi hicho sidhani kama kuna ukarabati wowote
wa uhakika uliofanywa na sasa hivi ndege zikitua pamoja na kwamba ni uwanja wa lami lakini utafikiri umetua kwenye matuta. Kwa hiyo, nawaomba Wizara wauangalie uwanja ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna masuala ya utafiti wa gesi yanakuwa yakifanyika pamoja na kwamba sasa hivi yamesimama. Kule kazi zinafanyika usiku baharini, uwanja hauna taa na kama mnavyofahamu Mtwara jua linaanza kutoka na linawahi kuchwa. Sasa siku nyingine mnaondoka abiria mnakaribia uwanja mnaambiwa uwanja umeshaingia giza mnarudi tena Dar es Salaam. Nawaomba waukarabati uwanja ule pia wauweke taa. Taa zinazotumika pale ni za wachimbaji wa gesi na hawaruhusu taa zao kwa sababu ni mobile wanaziweka pale tu panapokuwa na dharura na kwa maombi maalum. Kwa hali, ambayo tumefikia sasa hivi Mtwara kwa kweli tunaomba uwanja ule ukarabatiwe na uwekwe taa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kwa wale ambao wameenda Mtwara, lile jengo la abiria lipo ndani ya uwanja, nalo waliangalie waone uwezekano wa lile jengo kuliweka kama majengo mengine yalivyoojengwa. Haiwezekani jengo yaani unashuka kwenye ndege unaingia moja kwa moja kwenye jengo la abiria kwa sababu kwanza ni hatari kwa abiria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie tena kumpongeza Waziri pamoja na timu yake, niombe tu yale ambayo nimeuombea Mkoa wangu na kuiombea nchi yangu basi yafanyiwe kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi nami kuweza kuchangia. Napenda nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na watendaji wote wa sekta ya afya ambayo kwa kweli wanafanya kazi nzuri, ngumu na yenye changamoto kubwa lakini bado wanaonesha kuimudu, kwa hiyo napenda nimpongeze sana. Mheshimiwa Waziri amesoma hotuba yake vizuri ambayo inaonesha anajiamini lakini pia sekta hii anaijua vizuri. Ameonesha malengo bayana ambayo anakusudia katika bajeti hii kutatua kero ambazo ziko ndani ya sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunisaidia kunipatia gari la wagonjwa kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kitele, kwa kweli namshukuru sana. Pia nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri TAMISEMI kwa kutoa ufafanuzi kuhusu suala la upanuzi wa Kituo cha Afya Nanguruwe na Nanyumbu kuwa hospitali ya Wilaya, kwa sababu ilileta mkanganyiko mkubwa sana, kwa hiyo nawashukuru sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa maombi yafuatayo kwa Serikali. Ombi la kwanza ni kwamba bajeti hii iliyotengwa kwa kweli inatosha. Tunachoomba ni Wizara ya Fedha kuhakikisha kwamba pesa hizo zinakwenda kwa wakati ili yale tuliyoyapanga yaweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la pili, namwomba Mheshimiwa Waziri wa UTUMISHI, kwa dhati kabisa, kama ambavyo wanatoa vibali vya kuajiri Walimu basi awamu hii wajitahidi na Sekta hii ya Afya itolewe vibali vya kuajiri. Kwa kweli hali ni mbaya sana kwenye vituo vya afya hasa kutokana na huu uhakiki wa vyeti uliofanyika, vijijini kwetu huko kumeathirika zaidi kuliko hata mijini. Kwa hiyo tunaomba watoe vibali vya kuajiri Madaktari, Wauguzi pamoja na Matabibu. Kama wangesema sekta moja tu ipewe kibali, basi mimi ningesema ni sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi katika maombi ya mkoa wangu, Mkoa wa Lindi na Kanda ya Kusini kwa ujumla. Kila Kanda ina Hospitali ya Kanda ya Rufaa. Kanda ya Kusini ujenzi ulianza karibu miaka 10 iliyopita, lakini kwa miaka hii miwili mfululizo naona kama ujenzi umesimama inatengwa bilioni mbili na hiyo haitoki. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Ummy mdogo wangu afanye huruma kwa ndugu zake wa Kusini, atakapokuja basi atuambie ametuandalia nini cha matumaini ili kuhakikisha hospitali ile inakamilika kabla ya mwaka 2020 ili huduma ziweze kutolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti iliyopita Kamati ya Bajeti iliweka maombi na mapendekezo ya kuongeza tozo kwa ajili ya kupata pesa za kujenga vituo vya afya na zahanati katika kila Halmashauri. Lengo ikiwa ni kuboresha huduma za afya na pia kupunguza vifo vya akinamama na watoto. Serikali iliomba ipewe muda ifanye tathmini ili katika bajeti hii, waje na mpango mahususi wa kujenga kituo cha afya angalau kimoja kwa kila Halmashauri na zahanati angalau nne kila Halmashauri. Sasa upande wa TAMISEMI bahati mbaya wakati wa bajeti yao sikuwepo, lakini pia nimesoma kwenye makabrasha yao sikuona na upande wa sekta ya afya sioni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile tathmini Mheshimiwa Ummy nina uhakika wamemaliza. Kwa hiyo, tutaomba atakapokuja kutoa ufafanuzi au kutoa majibu atuambie, wametenga kiasi gani na baada ya kufanya tathmini wameona gharama ni kiasi gani na mwaka huu wanahisi ni kiasi gani kitatosha ili kuweza kujenga hivyo vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo pia nataka nilizungumzie ni suala la udahili wa kada zote za afya, iwe Madaktari, Wauguzi, Wafamasia kwa kweli uongezwe na sio udahili tu, lakini waajiriwe na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja
Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya eneo la Pori la Akiba la Selous kuwa Hifadhi ya Taifa ya Nyerere
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika azimio hili la kupandisha hadhi Pori la Selous kuwa Hifadhi ya Taifa. Niipongeze Serikali, nimpongeze Mheshimiwa Rais na nimpongeze Waziri pamoja na Kamati ya Maliasili kwa kuridhia pori hili kuwa hifadhi.

Mheshimiwa Spika, ni muda mrefu sana ambapo hili ombi lilikuwa linaenda linarudi, linaenda linarudi kwamba, Selous iwe hifadhi na sio Pori la Akiba. Kwa kuifanya kuwa hifadhi tutakuwa tunaiihifadhi zaidi Selous kuliko ambavyo sasa hivi liko pori ambalo uwindaji wa kitalii ndani yake mle unaruhusiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nipingane na Mheshimiwa Msigwa ambaye anasema hatujatoa taarifa UNESCO kwa sababu eti kuhifadhi tunahitaji ushirikiano wa kimataifa. Ndio tunahitaji ushirikiano wa kimataifa, lakini tunachokifanya sisi ni kupandisha hadhi, ina maana tunaendeleza uhifadhi zaidi, daraja kama ni uhifadhi tunaenda daraja la juu zaidi kuliko tulipo, tunachokifanya ndicho UNESCO inachokitaka. Tungeomba kibali cha UNESCO kama tungekuwa tunashusha hadhi kutoka kwenye pori na kuwa eneo la kawaida tu ambalo mtu yeyote anaweza akafanya kitu chochote.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuunga mkono hili wazo na niiombe Wizara ya Maliasili na Utalii suala hili la kupandisha hadhi Pori la Selous kuwa hifadhi liende sambamba na kutangaza vivutio vingine vilivyopo Kusini mwa Tanzania ikiwemo beach nzuri za Msimbati ambazo unaweza ukaenda na gari lako na ukaendesha kama ambavyo unaweza ukaendesha kwenye barabara yoyote ya lami kwa speed yoyote unayoitaka.

Mheshimiwa Spika, pwani hizi ziko chache sana duniani na kwa Afrika nadhani ni moja tu ambayo inapatikana Msimbati na pia tunayo hifadhi yetu kule ya Ruvula ambayo inazo bustani nzuri sana chini ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa vile umenipa dakika tano, naunga mkono Azimio la Kupandisha Hadhi Selous kuwa Hifadhi na pia tuiombe Serikali basi itangaze ukanda wote wa Kusini, ili watalii wakija Selous wawe na maeneo mengi zaidi, awe akifika Kusini awe amejitosheleza kwa kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha afya njema na kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili na mimi niweze kuchangia katika Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kumpongeza Waziri wa Mipango pamoja na Naibu wake, Katibu Mkuu pamoja na Manaibu wake, kwa kazi nzuri sana ambayo wanaifanya na pia ushirikiano ambao Kamati ya Bajeti wanaipatia. Napenda niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani ya Chama cha Mapinduzi iliahidi kujenga reli ya kati, sasa hivi tayari Mkandarasi wakujenga reli ya kati kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro yuko kazini na Mkandarasi wa kutoka Morogoro hadi Makutupora ameshapatikana, mkataba umesainiwa na kazi imeanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza tena Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi katika kuendeleza bandari zake. Nimeshiriki katika kuweka jiwe la msingi la upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam na sasa hivi Mtwara inajengwa gati yenye urefu wa mita 300. Nina uhakika kabisa ndani ya miaka ya miwili bandari zote mbili upanuzi ukikamilika kwa kweli sekta yetu ya usafirishaji hasa kwa njia ya bahari itakuwa imeboreshwa sana na uchumi wetu utakua kwa sababu korosho zetu na bidhaa nyingine kutoka katika Mkoa wetu wa Mtwara kama saruji kutoka kiwanda cha Dangote itakuwa hakuna matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia niipongeze pia Serikali yangu kwa hatua ambayo imefikia katika miradi ya kielelezo ikiwemo mradi wa Liganga na Mchuchuma, ambapo vile vivutio ambavyo wawekezaji walikuwa wanavitaka tayari wamepewa na kazi inaanza. Ninachotaka kuomba kwa Serikali yangu kwamba chuma kutoka Liganga makubaliano kipitie Bandari ya Mtwara, ili kiweze kupitia bandari ya Mtwara hatuwezi kusafirisha chuma kwa kutumia magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe ile reli ya kutoka Mtwara kwenda Liganga na Mchuchuma na Bamba Bay iharakishwe. Kwa sababu upembuzi yakinifu umekamilika, maeneo ambayo yatapita hiyo reli wananchi tayari wameshafanyiwa tathmini ya mali zao. Kwa hiyo, naomba ule mchakato mwingine uendelee ili pale ambapo uzalishaji kule utakuwa tayari na njia za kusafirishia ziwe pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuipongeza Serikali yangu kwa kuweza kulifufua Shirika letu la Ndege, kwa kununua ndege ambazo wananchi wa Mtwara na hata wa Dodoma kwa sababu unaweza ukatoka Mtwara ukafika Dar es Salaam ukaunganisha kuja Dodoma, ukatoka Dodoma ukaenda Dar es Salaam ukafika Mtwara na ukaenda kupata lunch kule kwa watani zetu kule Songea. Kwa kweli naipongeza sana Serikali yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tu kuiomba Serikali sasa hivi kwa kweli bei ya korosho ni nzuri sana na kule kwetu sasa hivi kila mtu ni furaha. Kwa vile wanaojishirikisha katika kilimo cha korosho ni wengi, manufaa yanayopatikana kipindi cha ununuzi wa korosho yanaenda kwa wananchi walio wengi. Sasa niiombe Serikali yangu tufike mahali tuache kuzisafirisha korosho zikiwa ghafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ule mpango wetu wa kupitia Mfuko wa Kuendeleza Zao la Korosho ambao ulipanga kujenga viwanda vitatu vya kubangua korosho, nimeona juzi wameanza kule Tunduru. Kwa hiyo, naomba na maeneo mengine ambayo walipanga wafanye ili tupate manufaa ya bei ya korosho iendane pamoja na ajira za viwandani kutoka katika viwanda vya korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza tena Serikali kwa kuanza mradi wa umeme wa Stigler’s Gorge, kama tunavyofahamu tunajenga reli ambayo itatumia umeme lakini tumeanza uchumi wa viwanda vyote hivyo vitahitaji umeme mkubwa, hivyo uanzishaji wa mradi wa Stiegler’s Gorge nadhani umekuja kwa wakati muafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza tena kwa Serikali tunayo gesi nyingi inayozalishwa, tunaomba pia itumike pia katika kuboresha viwanda vyetu na pia katika kuhakikisha tunapata umeme wa kutosha. Katika Mkoa wetu wa Mtwara tumeahidiwa kujengewa megawati 300, tunaomba huo mradi uharakishwe kwa sababu sasa hivi Mtwara kuna changamoto kubwa sana ya umeme. Tumeahidiwa kuletewa megawati 20, lakini megawati 20 nina uhakika ndani ya miaka wiwili ijayo zitakuwa hazitoshi, kwa hiyo suluhisho la kudumu ni megawati 300. Kwa hiyo, tunaomba miradi hiyo yote iende sambamba kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu za Shirika la Kuhudumia Watoto (UNICEF) zinaonesha ifikapo mwaka 2050 tutakuwa na watoto chini ya umri wa miaka 18 wafikao milioni 58. Watanzania kwa ujumla watakuwa milioni 108.

Je, tumejiandaa kuweza kuwasomesha watoto hao, kuweza kuwalisha watoto hao na kuweza kuwatibu watoto hao? Kwa hiyo, naiomba Serikali iweke mikakati ya kuhakikisha kwamba ongezeko la watu linaenda sambamba na ukuaji wetu wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumalizia kuna watu wanasimama wanaulizia pesa katika maeneo yao, lakini baadhi yao ni walewale ambao waliikataa bajeti iliyopita. Swali langu kwao, hizo pesa wanazoziulizia kwenda katka maeneo yao ni zile walizozikataa au kuna bajeti nyingine waliipitisha huko? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama una watoto wanne…

T A A R I F A . . .

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani wapiga kura wake wamemsikia na ndicho alichokuwa anataka. Swali langu nililoliuliza hakulijibu. Nimeuliza bajeti ambayo wao wanataka iende katika maeneo yao, ni ile waliyoikataa au nyingine?

T A A R I F A . . .

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mtu amepewa kazi yake, kuna waliopewa kazi ya kukusanya pesa na sisi tumepewa kazi ya kuidhinisha pesa. Kama wewe hujaidhinisha hizo pesa, unategemea zinafika kwao kwa mitindo gani? Wao hawakuidhinisha pesa na kama Waswahili wanavyosema asiyetwanga na asile, wao wamezikataa pesa, tupeni sisi tulioidhinisha pesa hiyo ndiyo taarifa ninayompa. Hata hivyo, nafurahi sana ukizungumza halafu wanawake kwa waume wakasimama kukupa taarifa maana yake taarifa yako imefika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kupitisha bajeti unaweza ukakataa, unaweza ukakubali, unaweza ukasema huna maamuzi. Sasa kwa wao ambao walikikubali hiki wakakataa kile wangesema sina maamuzi, lakini wao wamekataa, ndio maana nikasema watafute maneno ya kwenda kuwaambia wapiga kura wao ni kwamba wao bajeti waliikataa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja na naomba Waziri wa Fedha miradi yangu ambayo nimeiomba kwenye Jimbo langu nipelekewe pesa kwa sababu niliunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi ya kuzungumza. Nianze kwa kuwapongeza Wenyeviti wote wa Kamati kwa taarifa nzuri sana waliyowasilisha lakini pia bila kumsahau dada yangu Mheshimiwa Anne Kilango Malecela kwa hotuba yake nzuri sana ambayo ameimalizia hivi punde. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuipongeza sana Serikali yangu ya Awamu ya Tano na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri sana ambayo imefanya. Kuna watu ambao wanakaa wanasema tangu uhuru hatujafanya chochote, siwezi kuwakatalia kwa sababu wengi ni watoto wa miaka ya 80 na 90. Sisi ambao tumezaliwa tukiwa tunapita katika Mto Rufiji tukivuka kwa pantoni na sasa hivi tunapita katika Daraja la Mkapa katika Mto Rufiji tunajua wapi tulikotoka na kazi gani Serikali ya Chama cha Mapinduzi imefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niipongeze Wizara ya Miundombinu kwa kazi kubwa sana inayoifanya katika kupanua bandari zetu. Katika taarifa na hata hivi karibuni mimi mwenyewe nimeshuhudia uzinduzi wa upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam pamoja Bandari ya Mtwara. Kazi kubwa sana inafanyika kule kuhakikisha kwamba kule Mtwara tunaongeza Gati namba mbili ambalo litakuwa na urefu wa mita 300. Nina uhakika kabisa baada ya hapo korosho zetu na mizigo yetu ya Mtwara itakuwa inapita bila matatizo yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuanza ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka Mtwara - Newala - Masasi. Sasa hivi tayari mkandarasi yupo kazini, anajenga kipande cha Mtwara - Mivata zaidi ya kilometa 50. Niiombe Serikali yangu kile kipande kilichobaki basi mkandarasi mwingine sawa na ahadi ya Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli alivyoahidi kwamba vipande vyote vilivyobaki vitatafutiwa wakandarasi, hivyo tutafutiwe wakandarasi kwa sababu sisi Wabunge wa Chama cha Mapinduzi kazi yetu kuunga mkono bajeti yetu ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaomba ile miradi yetu itekelezwe na wale ambao wanaikataa bajeti wasishangae katika maeneo yao kuona mpaka sasa hivi hakuna kinachofanyika kwa sababu hakuna bajeti waliyoipitisha kwa ajili ya miradi katika maeneo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niunge mkono ujenzi wa reli kwa kiwango cha standard gauge ambao unaendelea sasa hivi kutoka Dar es Salaam kuja Morogoro na pia kutoka Morogoro hadi Makutupora. Pia suala la ujenzi wa viwanja vya ndege, naipongeza sana Serikali yangu na naipongeza sana kwa kulifufua Shirika letu la Ndege kwa kununua bombardier zile ambazo kwa kweli wote bila kujali vyama tunazipanda na tunazitumia kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nina changamoto moja tu ambayo nataka kuishauri Wizara ya Miundombinu, ndege zetu hizi zinalala au zina-park saa 10.00 au saa 11.00. Tatizo kubwa sana bombardier zinaweza kutua Uwanja wa Songwe, Kigoma, Mtwara, Bukoba na Songea lakini viwanja hivi vingi havina taa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe Waziri wa Miundombinu ahakikishe kwamba viwanja hivi vinawekwa taa ili ndege zetu hizi ziweze kutumika kwa ufanisi zaidi. Tunaweza kwenda Mtwara hata saa 4.00 au saa 6.00 usiku kama uwanja una taa lakini unakuta ndege zinakimbizana na jua, jua likizama na zenyewe zina-park. Pia viwanja hivi tukiweka taa tunaongeza hata usalama kwa ndege ambazo zinapita katika anga za kimataifa kukiwa na matatizo ya kutaka kutua wawe na viwanja mbadala vya kuweza kutua.

Mheshimiwa Naibu Spika, Viwanja vyetu vingi vinakosa sifa ya kuweza kutua usiku kwa sababu ya ukosefu wa taa. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa katika bajeti inayokuja ahakikishe viwanja vyote ambavyo bombardier inatua basi viwekewe taa ikiwemo pamoja na Kiwanja cha Mtwara. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa naipokea, ni kweli hizo pesa Mheshimiwa Rais amesema lakini lazima nikumbushe kwa sababu viwanja vilivyo kwenye huo mpango ni vingi, kwa hiyo, Waswahili wanasema lazima kamba kila mtu anavutia kwake. Kwa hiyo, naikubali taarifa na mimi namsisitiza Waziri kwamba zile pesa zilizotengwa hizo taa ziwekwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee na upande wa Wizara ya Nishati. Nataka nizungumzie deni la TANESCO. Deni la TANESCO ni la historia, tunalo kwa muda mrefu kwa sababu muda mrefu shirika letu lilitaka kubinafsishwa. Sasa yale madeni tukisema tuiachie TANESCO yenyewe iweze kuyalipa sidhani kama tunaitendea haki. Naishauri Serikali yangu ione uwezekano wa kuisaidia TANESCO kulipa yale madeni ili iweze kujikwamua na kuweza kutekeleza majukumu yake kwa uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba TANESCO inadai taasisi za Serikali lakini na yenyewe inadaiwa na taasisi kubwa ambayo inaidai TANESCO ni TPDC. TPDC inashindwa kutekeleza miradi yake mingi kwa sababu inapeleka gesi TANESCO na TANESCO anashindwa kulipa na TPDC naye anachukua gesi kwa watu. Kwa hiyo, naomba TANESCO isaidiwe kama tunataka ikimbie, tukiiacha yenyewe itakwenda kila siku ikitambaa. Kwa hiyo, nataka tuiwezeshe TANESCO kwa yale madeni aidha Serikali iyachukue au tuwasaidie kuyalipa au tuwasaidie kukopa ili waweze kujiendesha kwa tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka nichangie ni kwamba tuwe na gas master plan au mpango kabambe wa matumizi ya gesi kwa sababu sasa hivi kila mwekezaji anaweka kiwanda eneo ambalo analitaka yeye. Sidhani kama Serikali itakuwa na uwezo wa kumpelekea kila mtu gesi pale ambapo amejenga kiwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukitenga maeneo maalumu, tukaonyesha mpango kabambe wetu kwamba bomba la gesi litapita katika maeneo haya na yeyote anayetaka kutumia gesi akaweke kiwanda chake katika maeneo hayo, nina uhakika kabisa kwamba ndani ya muda mfupi tutakuwa na uwezo wa kuwafikishia gesi katika viwanda hivyo. Bila kuwapa maelekezo kila mtu akajenga anapotaka mwenyewe, tutakuwa na gesi nyingi lakini tutashindwa kuitumia kwa sababu gharama ya kuwafikishia watu gesi itakuwa ni kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimalizie kwa kuiomba Wizara ya Miundombinu kuunganisha barabara ya kutoka Mtwara - Kilambo kwa kiwango cha lami kwa sababu barabara hii inatuunganisha na nchi majirani zetu Msumbiji. Ni Sera ya Taifa kwamba barabara za Kitaifa ziunganishwe kwa kiwango cha lami. Natambua kwamba tayari kwa upande wa Mtambaswala tumeunganisha lakini watu wengi zaidi wanatumia kivuko cha Kilambo kwa ajili ya kwenda Mozambique kwa sababu ndiyo njia fupi zaidi kuliko upande mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuiomba Serikali wakati wa bajeti mara nyingi hapa tumekuwa na utaratibu wa watu kukataa kila bajeti, lakini inapokuja wakati wa utekelezaji walewale walioikataa bajeti ndiyo wanakuwa wa kwanza kulalamika kwamba kwao haijapelekwa. Mheshimiwa Rais aliomba kula kwa wananchi na alikuwa na ahadi zake na Wabunge tuliomba kura kwa wananchi tulikuwa na ahadi zetu. Kwa hiyo, zile ahadi zetu tutakuja kuulizwa sisi 2020 tumetekeleza kwa kiasi gani.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai na afya na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri ambayo ameitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo najielekeza katika masuala matatu, Suala la kwanza ni suala la Hospitali ya Rufaa kanda ya kusini, ambayo tayari ujenzi wake ulishaanza, mapokezi tayari, OPD umeshakamilika, ukuta umejengwa lakini kwa zaidi ya miaka miwili mfululizo pesa zinawekwa kwenye bajeti lakini hazitolewi. Sasa kama makusanyo ni matatizo basi wote tugawiwe sawa, sio wengine wanapewa asilimia 80, wengine asilimia 60, wengine sifuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la pili ambalo nataka kulizungumzia ni suala la uwanja wa ndege wa Mtwara. Kwa zaidi ya miaka mitatu umekuwa ukisindikiza viwanja vingine. Tumekuwa tukiwekewa pesa tukiambiwa kwamba utawekewa taa na utafanyiwa ukarabati kwa sababu upembuzi yakinifu umekamilika, lakini kila mwaka pesa ile inatengwa na inatoka sifuri. Kwa hiyo, nataka niombe kama hakuna pesa ambayo inatakiwa kupelekwa katika kitu chochote aidha hospitali au uwanja wa ndege wasituwekee kiini macho halafu hatuwekewi kitu chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu ambalo ndio ningetaka nichukue muda mrefu ni suala la pembejeo la zao la korosho. Korosho kwetu sisi wananchi wa Mtwara, Lindi na Ruvuma, ni uchumi lakini pia ni siasa. Katika miaka mingi iliyopita katika mkoa wetu wa Mtwara tumekuwa na
utaratibu wa kuwa na Mifuko yetu ya ngazi ya Wilaya na Mikoa kwa ajili ya pembejeo za mazao yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017 Mheshimiwa Waziri wa Kilimo akaja akawatangazia wananchi kupitia mkutano wa wadau wa korosho kwamba pembejeo zinatolewa bure na akaelekeza wale ambao waliokuwa wamechangia kupitia katika Mifuko yao werejeshewe zile pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna Mbunge ambaye aliomba tupewe pembejeo bure na hata kwenye kikao vya wadau baadhi ya wananchi walikuwa wanapinga wakiamini kwamba suala hili halitakuwa endelevu. Cha kusikitisha mpaka sasa hivi hatujui pembejeo za korosho zitapatikana kwa utaratibu upi mpaka dakika hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upuliziaji wa zao la korosho unatakiwa kuanza mwezi wa tano mara nyingi na kila baada ya siku 21 na unatakiwa urudie mara tano mfululizo kila baada ya siku 21 na ukichelewa mara ya kwanza maua yanapotea na uzalishaji unashuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ametuambia hapa kwamba kwa mara ya kwanza kilimo kimeongezeka kwa asilimia sita ukuaji wa pato linalotokana na kilimo imekuwa kwa asilimia 3.6, kwa mara ya kwanza. Kilichochangia ukuaji huo ni zao la korosho, kutokana na uzalishaji kuongezeka lakini pia kutokana na bei ya korosho kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku zote tumekuwa tukisema kwamba uchumi wa nchi unakua kwa asilimia saba mfululizo kwa zaidi ya miaka 10, lakini ukuaji ule hauonekani kwa wananchi kwa sababu sekta zinazokuwa si sekta ambazo zinaajiri wananchi wengi na sekta inazoajiri wananchi wengi ni kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uelewa wangu na kwa ufahamu wangu na kwa uchumi wangu ambao niliusomea, nilitegemea Serikali yangu kwa kuwa zao la korosho mwaka jana lilifanya vizuri, kwa hiyo, mipango ya pembejeo na maandalizi mengine yangefanyika mapema na wakulima wangekuwa na uhakika kwamba kwenye pembejeo za korosho wanazipata kwa utaratibu upi na wanazipata lini. Sasa zao ambalo limezalisha vizuri ndio ambalo mwaka huu tumeamua hatutaki kuwekeza kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli nioneshe masikitiko yangu. Zao la korosho na mazao mengine tulipitisha sheria hapa tukaanzisha Mifuko ya kuendeleza mazao yakiwemo korosho, kahawa, pamoja na pamba na mazao mengine. Mfuko wa Korosho mpaka sasa hivi tunavyozungumza una zaidi ya bilioni 88 za msimu 2016/2017 kwa ajili ya kuendeleza zao la korosho, ikiwa ni pamoja na ubanguaji, utoaji wa miche bora, suala la pembejeo na suala la utafiti katika kituo chetu cha Naliendele, lakini pesa hizo mpaka sasa hivi hatuelewi. Pesa hizo tulitunga sheria hapa ya mwaka 2009 na marekebisho yake ya mwaka 2011. Sheria haijafutwa na Bunge hili, tunaanzaje kuzuia pesa hizo wakati sheria hatujabadilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, msimu wa mwaka 2016/2017 zao la korosho, korosho zilizalishwa tani 265,237,845 zenye thamani ya Sh.871,462,989,287. Msimu wa 2017 uzalishaji umeongezeka mpaka tani 313,530,700 zenye thamani ya shilingi trilioni moja, kutoka bilioni 871 mpaka trilioni 1.189. Wananchi wamepata zaidi ya trilioni moja, hiyo trilioni moja imeenda kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa mkoa wa Mtwara peke yao wamepata bilioni 705,399,000,000. Halmashauri msimu wa mwaka 2017 zimepata bilioni 8.2, msimu 2016/2017 walipata bilioni 11 kwa sababu viwango vya tozo vimepungua. TRA yenyewe ilipata msimu wa 2016 zaidi ya bilioni 103 kwenye zao la korosho. Hivi kwa mafanikio haya nilitegemea Serikali yangu itumie kila aina ya juhudi kuhakikisha kwamba zao hili sasa linawezeshwa ipasavyo ili kuhakikisha kwamba uzalishaji unaongezeka mwaka hadi mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nioneshe masikitiko yangu, tangu mwaka 2017 mwishoni mwezi Desemba, tumeenda kumtembelea Waziri wa Fedha Wabunge wote wa Mtwara zaidi ya mara mbili. Tumeenda kwa Katibu Mkuu, mara ya kwanza wakatuambia kwamba pesa zipo msiwe na wasiwasi tatizo ni kwamba hii sheria tangu imetengenezwa haina kanuni. Tumekaa tukapitisha kanuni. Tukaambiwa Bodi hawana mpango kazi wala mpango wa manunuzi, wametengeneza imeenda. Sasa hivi tunaambiwa inatoka milioni kumi na bilioni kumi yenyewe kizungumkuti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoka kwenye korosho, anaijua korosho naomba korosho isimfie mikononi mwake. Anafahamu katika utaratibu wa kawaida sasa hivi meli za kuleta pembejeo zinapaswa kuwa zimefika. Hata hivyo, ninachoomba Waziri wa Kilimo na Waziri wa Fedha waende Mtwara, waende Lindi, waende Ruvuma wakawaambie wananchi kwamba pembejeo mwaka huu hawatapata kwa sababu walituahidi watazitoa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema nami kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili kuweza kuichangia bajeti hii muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano na kumpongeza Waziri pamoja na Manaibu wake na watendaji wote wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kuishukuru Serikali kwa upanuzi wa Bandari ya Mtwara ambao unaendelea vizuri. Ni imani yangu kwamba upanuzi ule utakamilika kwa wakati na hivyo kuwezesha huduma za usafirishaji katika mkoa wetu hasa za zao la korosho kwenda kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia niishukuru Wizara hii kwa kuanza upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Mtwara. Juzi nimetoka Mtwara nimeona magari pale yapo, nina imani kabisa kwamba kazi ile itaanza kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia katika kitabu cha hotuba na nimeona kazi zitakazofanyika. Napenda kupendekeza kwamba pamoja na kazi walizojiwekea ikiwa ni pamoja na kuweka taa katika uwanja ule, naomba pia suala la kujenga jengo la abiria na lenyewe liwekwe kwa sababu jengo lililopo lipo ndani ya uwanja. Kwa hiyo, ningeomba Mheshimiwa Waziri, yeye mwenyewe ameenda na ameona na pia lile jengo lililopo ni dogo na halitoshi kutokana na upanuzi ambao unataka kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda niipongeze Serikali kwa kununua ndege, sasa hivi tuna ndege ya tatu. Nina uhakika kabisa kwamba ufanisi wa Shirika la Ndege la Tanzania utakuwa ni wa kiwango cha juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa masikitiko yangu kwamba Bombadier zilikuwa zinakuja Mtwara lakini sasa hivi huu ni mwezi safari za Mtwara zimefutwa eti kwa sababu Kiwanja cha Ndege cha Songea ni kibovu. Sasa Kiwanja cha Ndege cha Songea kimeanza juzi, Kiwanja cha Ndege cha Mtwara kilikuwepo enzi na enzi na kilikuwa kinafanya kazi bila Kiwanja cha Ndege cha Songea. Sasa kama Kiwanja cha Ndege cha Songea kina matatizo, hakuna sababu yoyote ya kufungia ndege za ATCL kwenda Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mnasema abiria ni wachache ni kutokana na ratiba zenu ambazo kwa kweli haziwavutii abiria. Mnaunganisha abiria wa Mtwara na Songea. Unaruka Dar es Salaam saa 6.30 unafika Mtwara saa 9.15, zaidi ya saa 2.45 wakati kutoka Mtwara mpaka Dar es Salaam ni dakika 50 kwa Bombadier. Hivi unafikiri kweli utaweza kushindana na Precision?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kawaida sisi kama ni kuunganishwa, tunaunganishwa na abiria wa Hahaya kule Comoro kwa sababu kutoka Comoro mpaka Mtwara ni dakika 25 mpaka dakika 30. Kwa hiyo, niwaombe warejeshe ndege Mtwara lakini watuunganishe na Comoro na nawahakikishia watajaza ndege kwa abiria kutoka Mtwara kama watakuwa na ratiba zilizo…

T A A R I F A . . .

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, huyo ni mtani wangu, kwa hiyo sipendi kubishana na mtani wangu lakini ukweli anaujua na ninaozungumza nao nadhani wananielewa. Isipokuwa tu labda nimsaidie niseme uboreshaji wa Kiwanja cha Songea ufanyike kwa kasi ya hali ya juu ili mtani wangu naye aendelee ku-enjoy kwenda na ndege kwa sababu kwa sasa hivi hata wakiturudishia sisi hawezi kupata. Kwa hiyo, uboreshaji wa Kiwanja cha Ndege cha Mtwara uende sambamba na Songea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nilizungumzie ni suala la uunganishaji wa barabara zetu. Sera ya nchi ni kuunganisha barabara za nchi na nchi, lakini sasa hivi katika Mkoa wa Mtwara tunayo barabara ya kutoka Mtwara - Mozambique kupitia Kilambo ambayo ndiyo barabara inatumiwa na wananchi wengi wanaokwenda Mozambique.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Wizara hii imetuwekea kivuko pale cha kisasa na watu wanatumia sana lakini barabara hii bado haijajengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, niiombe Serikali iijenge barabara ya kutoka Kilambo kwenda Mtwara kwa kiwango cha lami kwa sababu inatuunganisha na majirani zetu wa Mozambique na ni sera ya nchi kuunganisha nchi kwa nchi kwa barabara za lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuiomba Serikali kuharakisha mchakato wa kujenga reli ya kutoka Mtwara kwenda Mbamba Bay na matawi yake yanayokwenda Liganga na Mchuchuma. Upanuzi wa Bandari ya Mtwara kama hakutakuwa na reli itakuwa ni kazi bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mtwara tuna kiwanda kikubwa sana cha Dangote, magari ya kiwanda kile hakuna lililo chini ya tani 30. Sasa hivi zile barabara zetu za udongo ni mahandaki. Ndiyo kusema bila kuwa na reli tunategemea Dangote achukue makaa ya mawe kutoka Ngaka na saruji isafirishwe kupelekwa Songea na mikoa mingine na tuchukue chuma na makaa ya mawe ya Liganga na Mchuchuma kwenda Mtwara bila kuwa na reli barabara zile kwa kweli zitaharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza sana Serikali kwa kuikamilisha barabara ya kutoka Dar es Salaam – Songea. Sasa hivi watani zetu wale wanaoogopa milima wanaitumia sana, mabasi karibu yote ya Songea yanapita barabara ya kutoka Mtwara ya Kilwa Road – Masasi - Tunduru - Ruvuma lakini bila kuwa na reli nina uhakika barabara ile itadumu kwa muda mfupi tu. Sasa hivi kwa ushahidi barabara ya Masasi – Mangaka - Tunduru imeshaanza kuharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe mchakato uharakishwe kuhakikisha kwamba ujenzi wa reli ile unakamilika. Upembuzi yakinifu ulishakamilika, tathmini ya mimea ya maeneo inapopita ilishakamilika na tunachoomba siyo lazima tutumie pesa za Serikali, tunaweza kujenga barabara ile kwa njia ya PPP na njia hii ndiyo itakayotusaidia pia kupunguza deni la Serikali kwa sababu hatutakopa. Tunaweza tukaingia ubia, sisi tukaweka mchango wetu na mwekezaji akaweka mchango wake na bado tukanufaika na matunda ya reli ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimalizie kwa kuipongeza Serikali kwa kuanza ujenzi wa barabara ya kutoka Mtwara – Nanyamba - Tandahimba-Newala - Masasi. Sasa hivi tuko katika kilomita 50, nimeangalia katika kitabu cha bajeti sijaona ile barabara kuongezewa pesa. Mheshimiwa Rais alituahidi kwamba akishinda vipande vilivyobaki atatafuta wakandarasi wengi zaidi ili barabara ile ikamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Profesa Mbarawa asimuangushe Rais wetu, nia yake ni njema kwa wananchi wa Mkoa wa Mtwara na Lindi kwa sababu barabara ile itakwenda mpaka Nachingwea na kutuunganisha pia na mikoa ya jirani zetu, watani zetu Songea, naomba aitekeleze kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Kumi na Moja wa Bunge
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenijalia uhai na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako tukufu na kuweza kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu.

Pia nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Spika kwa kuanzisha Kamati hii, lakini pia utaratibu wa kuwasilisha taarifa hii mara mbili kwa mwaka, kwa sababu imekuwa na mchango mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyofahamu kwamba sheria ndizo ambazo Bunge tunashiriki kwa kiasi kikubwa katika kuzitunga, lakini kanuni zinatungwa na Mawaziri na zinaanza kutumika sisi tunakuja baadae kuziona. Kwa hiyo, ukiangalia kwa kiasi kikubwa sheria nyingi kwa kuwa, zinakuwa zimepitia kwa wadau wengi unaweza ukakuta hata kama kunakuwa na mapungufu yanakuwa ni machache sana. Kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Mawaziri wakati wa kuandaa kanuni si vibaya tukashirikisha wadau mbalimbali, ili na wenyewe wakatia mchango wao na wakaweza kutusaidia katika kuziboresha kanuni zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo Sheria yetu ya Madini ambayo tuliipitisha mwaka jana na pia tukawa na kanuni zake; Sheria ya Usimamizi wa Mapato ya Mafuta na Gesi. Sasa katika kanuni ukiangalia suala la local content na suala zima la indigineous bank na ndigineous company, ukiangalia pale unakuta kunakuwa na matatizo makubwa sana. Nia ya sheria ni nzuri, lakini inavyokuja kanuni unakuta sasa ile nia nzuri inapotea. Lengo la kuhakikisha kwamba, tunakuwa na local content siyo kwa vile ambavyo imetafsiriwa katika kanuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaposema kwamba, kampuni ya madini itawekeza akaunti zake katika indigenous bank na ukatoa tafsiri ya indigenous bank ambayo inaitoa CRDB, inaitoa NMB na naitoa NBC, benki zinazobaki kwa kweli, hazina uwezo hata hizo kampuni zikisema yanataka kukopa, lakini hata uwezo wake ule wa kuhimili kwa sababu baada ya hapo zitabaki labda Mwanga Community Bank, Mufindi Community Bank au labda Azania, ndizo ambazo utazikuta zinaendana na yale masharti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuwa kanuni ikitoka inachukua muda mrefu sana kuja kurekebisha, mimi nadhani ni vizuri sana Waheshimiwa Mawaziri wanapozitunga zile kanuni hata wakaishurikisha Kamati ya Sheria Ndogo wakazipitia kabla ya kuzitangaza katika Gazeti la Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika kabisa kwamba zitakuwa ni kanuni nzuri sana kwa sababu hatutegemei kanuni izizidi sheria, lazima sheria iwe juu ya kanuni. Kwa hiyo, hilo lilikuwa ni pendekezo langu la kwanza, kwamba Waheshimiwa Mawaziri wanapotunga kanuni, wala sio vibaya waka-share na Kamati Ndogo, lakini pia wakawashirikisha wadau mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiachia suala la benki, mfano indigenous company, Shirika kama PUMA Serikali ina hisa 50%. Ndiyo kusema PUMA ikinufaika na Serikali imenufaika na wananchi wananufaika, kwa sababu Serikali inasimama kwa niaba ya Watanzania. Sasa kwa kanuni ile sasa inaitoa PUMA kufanya kazi na migodi ya dhahabu au na migodi mingine, kwa sababu PUMA sasa inakuwa sio indigenous company kwa sababu share za Serikali au share za Watanzania kupitia Serikali ni 50% tu. Kwa hiyo, niombe wakati tunavyotunga kanuni, nia ni nzuri, lakini tuwe tunaangalia hivi tunavyosema indigenous company au indigenous bank ni zipi tunazozikusudia na kama sisi tutanufaikaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kwa kiasi kikubwa kampuni zetu, sekta binafsi katika nchi yetu ni change, kwa hiyo tunategemea pale ambapo Serikali ipo, imeingia ubia, ndio wananchi wapo, Serikali ikinufaika Wananchi tumenufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo pia nilitaka nilichangie, tumesikia kwamba kumekuwa na matatizo ya uandishi katika baadhi ya kanuni na wakati mwingine hata sheria ndogo zinazotungwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Hata hivyo wakati mwingine makosa yale yanajitokeza kutokana na uchache wa rasilimali watu katika ofisi zetu na wakati mwingine na wingi wa kazi uliopo. Mfano kama sasa hivi unakuta tuna Halmashauri 185, useme tu nusu yake wamepeleka Sheria zao Ndogo TAMISEMI na zinahitajika kwa haraka, umepeleka Sheria Ndogo 80 au 90, watumishi waliopo je, wanaendana na kazi iliyopo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali nayo tuhakikishe kwamba, tunaijengea uwezo kwa maana ya kwamba, watumishi, rasilimali watu, lakini pia na kuziwezesha kwa sababu tunazo sekta zinazoibukia, masuala ya gesi na oil. Wengi wa wanasheria wetu wamesoma, lakini wanasoma mambo hayo hayakuwepo, lazima tuwajengee uwezo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nikushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi kubwa sana wanayoifanya. Wote ni mashahidi, tunafahamu tulikotoka kwa kiasi gani Wizara hii ilikuwa na changamoto nyingi sana na kwa kiasi gani wameweza kuzifanyia kazi changamoto nyingi ambazo zilikuwa zinaikabili Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Spika, kuna mageuzi makubwa sana ambayo Wizara imeyafanya. Sasa hivi karibu maeneo mengi master plan au mipango kabambe ya ardhi inaandaliwa mpaka katika ngazi za halmashauri kwa hiyo, napenda sana. Wamekuwa wakiandaa mipango ya makazi na vijiji, wamekuwa wakisimamia udhibiti na uendelezaji wa miji. Pia niwapongeze kwa kutwaa baadhi ya maeneo ambayo kwa kiasi kikubwa yalikuwa ni mashamba pori.

Mheshimiwa Spika, nishukuru sana kwa sababu haiwezekani mtu anachukua eneo anasema anataka kuwekeza, kufanya shamba, anachukua zaidi ya miaka 17 hajaotesha mti hata mmoja, hajaendeleza, hajafanya hilo shamba na bado tuendelee kumuangalia. Kwa kweli ninaipongeza sana hii Wizara.

Mheshimiwa Spika, pia, ninapongeza hasa ukizingatia taarifa ya Kamati, kamati wameipongeza sana Wizara yao na wamesema katika mapendekezo yale mengi ambayo waliipa Wizara yamefanyiwa kazi. Sioni kwanini Wizara hii ijadiliwe siku mbili, haki yake ilikuwa tujadili leo, ifike jioni tumalize tuangalie yajayo ambayo ni kukaribisha Eid na wale wanaoenda mbali waweze kwenda lakini vinginevyo kazi kubwa sana Wizara imefanya kikubwa ni kuishauri Serikali iendelee kuipatia fedha Wizara iweze kufanya kazi ambazo zinatakiwa.

Mheshimiwa Spika, jingine ambalo nilitaka kushauri. Wizara inajenga nyumba nyingi sana kupitia National Housing na mfuko wa watumishi wa umma lakini zile nyumba zenyewe pia waziweke kwa makundi, tusiweke tu za gharama nafuu. Kuna nyumba zingine zinajengwa karibu karibu hata ukikohoa jirani yako anakusikia. Watakapojenga nyingine basi waziweke kwa tabaka, waweke zile za bei nafuu lakini pia waweke na daraja la kati na wale wa juu pia wawafikirie kwa sababu unaweza hizi za gharama nafuu ukajenga asilimia 60, zile nyingine asilimia 20.

Mheshimiwa Spika, mwisho nirudie tena kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu ikiwezekana hii bajeti leo basi tuibariki kwa sababu kazi kubwa wameifanya na wanaendelea kuifanya Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja kwamba bajeti hii tuimalize leo. (Makofi)
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa fursa hii niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Fedha. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwigi wa rehema ambaye ameniwezesha afya njema na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako tukufu kuweza kuichangia bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, napenda nianze kwa kumpongeza Waziri wa Fedha na Naibu wake pamoja na taasisi zilizo chini yao. Pamoja na pongezi hizo ningependa kushauri katika maeneo yafuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza ni suala la Tume ya Mipango. Tume ya Mipango ipo kisheria na ni chombo pekee ambacho katika nchi mbalimbali ndio kimekuwa tegemeo la kuishauri Serikali katika mipango yake ya nchi. Na nchi nyingi zilizofanikiwa zimepitia chombo hiki ambacho aidha ni Tume ya Mipango au ni vyovyote wanavyoita, lakini ambacho kinahusika na masuala ya mipango na wengine wanaitwa think tank. Tume ya Mipango inapaswa kuwa chombo huru ambacho kinakuwa juu ya Mawaziri wote akiwemo na Waziri wa Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ndio maana tuliwahi kuwa na Wizara ya Fedha na Wizara ya Mipango. Na pia tumewahi kuwa na Waziri wa Nchi ndani ya Ofisi ya Rais, anayeshughulikia Mipango; na ndio maana tukapata Mpango wa Kwanza wa Maendeleo wa Taifa, ambao ulikuwa na lengo la kuondoa vikwazo vya maendeleo na tukawa na Mpango wa Pili ambao wenyewe unajielekeza katika Uchumi wa viwanda. Na tulikuwa na Mipango miradi ya kielelezo ambayo ilikuwa inasimamiwa na Tume ya Mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia katika bajeti ya mwaka huu iliyotoka, hata lile jina miradi ya kielelezo limepotea, miradi ya kimkakati imetoweka kwa sababu Tume iliyokuwa inashughulikia masuala hayo haipo. Niombe Serikali yangu, chombo kile au tume ile irudi na ikiwezekana ili iwe huru iwe Tume ndani ya Ofisi ya Rais. Iwajibike moja kwa moja kwa Mheshimiwa Rais na iwe inatoa maelekezo kwa Wizara zote ikiwemo na Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia sasa hivi Wizara ya Fedha inaangalia zaidi kukusanya kuliko kuanzisha miradi au mipango ambayo itakuza uchumi na kuiwezesha Wizara ya Fedha kuweza kukusanya. Kwa sababu suala la mapato au revenue ni function ya price times quantity. Sasa badala ya kuongeza tu hiki kiwango cha tozo kwamba mwaka huu umetoza shilingi 10, mwakani shilingi 20, mwakani shilingi 30 ongeza uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuongeze viwanda viwe vya vinywaji, viwe vya saruji unaweza ukabaki na tozo yako ile ile lakini ukakusanya zaidi na ndio hapo ambapo tunaitaka Tume ya Mipango ili iweze kutushauri kama ni viwanda, ni viwanda vya aina gani ambavyo vitachangamisha uchumi wetu kwa haraka zaidi na hivyo kuiwezesha Serikali kuweza kupata makusanyo mengi zaidi na kwa haraka zaidi. Tukiendelea tu kupandisha kodi, kodi, kodi kila siku tunakula mitaji, tunaua biashara, makusanyo yanashuka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo nilipenda nichangie ni suala la ubia wa Serikali na sekta binafsi. Tumezungumzia madeni ya Serikali, madeni ya Serikali hakuna ubishi kwamba mpaka sasa hivi ni himilivu kwa vigezo vyote, lakini tunataka yaendelee kuwa himilivu kwa vipindi vyote. Kitu ambacho kitatusaidia deni letu liendelee kuwa himilivu ni kwa kuangalia miradi ile ambayo iko kimtizamo wa kibiashara, basi Serikali iingie ubia na sekta binafsi ili tupunguza kukopa. Tukiingia ubia na sekta binafsi kama Serikali tutachangia sehemu yetu lakini pia tutaweza kupitia ubia wetu kuongeza uzalishaji na pia kuongeza mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, tangu tulivyopitisha Sheria ya PPP mpaka sasa hivi ukiacha Mradi wa DART ambao miundombinu imejengwa na Serikali kwa asilimia 100 lakini tumeingia ubia kwenye uendeshaji. Hakuna mradi mwingine ambao unaonesha tayari Sheria ya PPP imefanikiwa.

Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri Wa Fedha tuharakishe mchakato, tunayo miradi mingi hata ukipitia kwenye hotuba mingi ambayo imeorodheshwa, lakini yote hiyo iko kwenye upembuzi yakinifu. Nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha huo upembuzi yakinifu basi uharakishe ili ile miradi itekelezwe na hiyo ndio itakayotusaidia. Pesa ndogo tulizonazo zipelekwe kwenye sekta ya afya, zipelekwe kwenye elimu, zipelekwe kwenye miradi ile ambayo sekta binafsi wanaiona haivutii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo pia nilitaka nilichangie ni suala la michezo ya kubahatisha. Ukiangalia kwenye kitabu hiki cha Waziri wa Fedha mwaka huu kumekuwa na mafanikio makubwa sana yamepatikana mapato mengi sana kutokana na michezo ya kubahatisha, lakini mafanikio haya tulipata shida sana mwaka jana Bodi ya Michezo ya Kubahatisha kutukubalia kwanza kodi hii kukusanywa na TRA, lakini pia kuongeza tozo ambazo zilikuwa zinatozwa mpaka Mwanasheria Mkuu wa Serikali alivyowauliza mimi mbona ninawashangaa kwamba Kamati inataka muongeze kutoza ninyi mnakataa ndipo walipokubali, lakini leo wote tunasherehekea mapato kwamba hii michezo ya kubahatisha imeongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kwenye michezo ya kubahatisha Serikali inaweza ikakusanya pesa nyingi zaidi kuliko inavyokusanya sasa hivi, kuna makampuni zaidi ya 46 yanayojishirikisha katika hii michezo, lakini ukiziangalia makusanyo hayo yote yanatoka katika makampuni matatu tu, yapo makampuni yanayocheza michezo inayofanana lakini kila mtu anatozwa kiasi chake.

Katika baadhi ya maeneo watoto wetu wadogo wanaenda kwenye ku-bet huko kwenye vibanda lakini Serikali pale inapata shilingi 32 tu kwa mwezi tungependa iongezwe kiasi hiki. Waswahili wanasema ukitaka kula nguruwe basi mle aliyenona, si wengine hii ni kamari, lakini kwa vile Serikali imetaka iende basi kamari hiyo inufaishe zipatikane pesa za kutosha watu wapate maji, wapate barabara, wapate kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna watu wanapata kwa mwezi zaidi shilingi bilioni tano wanatoa shilingi milioni 200 tu kwa Serikali. Tunaomba eneo hili bado Serikali ifanyie kazi tulishapeleka mapendekezo muda mrefu ya kuitaka Serikali iongeze kwa baadhi ya watu wanakuwa-charged asilimia
12; asilimia sita tukasema waongezewe lakini mpaka sasa hivi hatuoni kama Serikali ina nia ya kuongeza katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema nami kuweza kusimama mbele ya Bunge tukufu ili niweze kuchangia hoja mbili ambazo zimewasilishwa katika Bunge letu Tukufu. Pia napenda niwapongeze Wenyeviti wote wa Kamati kwa taarifa nzuri sana ambazo wameziwasilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia maeneo machache sana, kwanza nikianza na taarifa ya mwaka ya Kamati ya Uwekezaji Mitaji ya Umma (PIC). Niwapongeze wote waliochangia nami niungane nao katika kuiomba Serikali kuziongezea mitaji taasisi zetu ambazo ziko chini ya Msajili wa Hazina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ndio maduka yetu, hivi ndio viwanda vyetu ambavyo Serikali inaweza ikatuongezea pato letu la Taifa na katika biashara yoyote ni lazima uwekeze ndipo uweze kuvuna. Kwa hiyo, kwanza nashauri Sheria ya Msajili wa Hazina ipitiwe upya ili kuweza kumwezesha Msajili wa Hazina kufanya kazi zake kwa ufanisi. Pia napendekeza ikama katika Ofisi ya Msajili wa Hazina iongezwe na pia katika kuipitia sheria napendekeza ikiwezekana tuanzishe Mfuko wa uwekezaji ambao wenyewe ndio utakuwa unatoa mitaji kupeleka katika mashirika yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo mashirika ambayo tumeingia ubia, PUMA tuna ubia lakini tunayo mashirika mengi kama TPDC imeingia ubia na mashirika mengi kama MMP na pia tumeingia ubia sigara, tumeingia ubia ALAF, lakini katika ubia ule uwekezaji wetu kidogo ni mdogo sana ukilinganisha na wabia wenzetu. Sasa kwa kuwekeza kidogo inapelekea mapato yetu au gawio letu kwa kweli kuwa kidogo kwa sababu tunawekeza kidogo. Kwa hiyo napendekeza tuwe na mfuko wa uwekezaji ambao utamwezesha Msajili wa Hazina kuweza kutoa mitaji katika yale mashirika ambayo anayasimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo nataka nichangie ni kuhusu suala la ATCL. Niungane na wenzangu kuipongeza Serikali yetu kwa kuwa na Shirika letu la Ndege. Napenda niwaambie kwamba Shirika la Ndege tusiangalie balance sheet ya shirika kwamba, faida tumetumia kiasi gani tunapata kiasi gani, tuangalie faida katika uchumi mpana, idadi ya watalii walioletwa, uwekezaji utakaokuja. Katika kuthibitisha hilo nendeni mkaangalie Shirika la Emirate ambalo sasa hivi kila mtu analipigia mfano, wakati linaanza lengo lake kubwa halikuwa kuweka faida. Lengo lilikuwa ni kuifanya Dubai iwe kituo cha uwekezaji, iwe kituo cha utalii. Sasa hivi Dubai asilimia 20 ya mapato yake...

T A A R I F A

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unitunzie muda wangu, taarifa naipokea, na ndio maana nilikuwa nasema naungana na Serikali kwa kununua ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu leo labda China hata Tanzania hawaijui, lakini siku ndege yetu ikitua Guangzhou, watu wataanza kujiuliza, Tanzania iko wapi, kuna nini, kuna vitu gani vinapatikana huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dubai kuanzia Disemba mpaka inafika Machi hoteli zote zimejaa, mji umejaa na pato la Taifa la Dubai kwa mwaka 2018 asilimia 20 lilichangiwa na utalii na utalii huo ulibebwa au watalii hao walibebwa na Shirika la Emirate na walichangia katika uchumi mpana kwa watalii kwenda pale. Kwa hiyo, niwaombe ile habari ya kusema sijui tumenunua hivi, tumepata vile, hiyo ni biashara ya machungwa, lakini unavyoangalia biashara kama ndege unaangalia katika uchumi mpana, idadi ya watalii shirika litatangaza nchi yetu na italeta multiplier effect kubwa sana kuliko ambavyo watu wanafikiria, lakini pia nina imani kabisa shirika letu litakuja kufanya faida na kupunguza gharama za usafirishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Mtwara ambako Bombadier zimekatiza kwa sababu ya Ruvuma, nauli ya ndege kwa kutumia Precision ni kubwa kuliko eneo lingine lolote ndani ya Tanzania hii. Kwa hiyo, kwa kuwa na Shirika letu pia tunasaidia kupunguza gharama za usafiri wa anga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.4) wa Mwaka 2016
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Kwa haraka niwapongeze Waheshimiwa Wabunge wote walioteuliwa na Mheshimiwa Rais pia Mheshimiwa Mbunge aliyeshinda katika mapambano makali kule Dimani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda nikipongeze Chama changu cha Mapinduzi kwa kuchukua karibu Kata zote katika Uchaguzi ule wa Madiwani. Hiyo imeonesha kwamba sasa kazi imeanza na njia huko mbele ni nyeupe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niende kwenye muswada ambapo ninataka niangalie tu katika Marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Mapato (Income Tax Cap. 332).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sheria iliyokuwepo uamuzi wa kusamehe kodi ulikuwa mikononi mwa Waziri wa Fedha, katika marekebisho ambayo tunataka kuyafanya sasa hivi ni kwamba kwa ile miradi ambayo tunaona kwamba ni ya kimkakati na ina maslahi ya Kitaifa, basi maamuzi takwenda kufanywa katika Baraza la Mawaziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina pingamizi lolote na hicho, lakini kimsingi maamuzi ya Baraza la Mawaziri hayawezi kupelekwa kwenye Kamati yoyote na hayawezi kuhojiwa na Kamati yoyote, kama ambavyo vile tulikuwa tunaweza kumhoji Waziri wa Fedha pale ambapo misamaha inaenda, au akivuka kile kiwango ambacho tulikuwa tunakitaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wasiwasi wangu ni kwamba kwa kufanya katika Baraza la Mawaziri na tumesema kwamba tutaangalia miradi ile ambayo ni ya kimkakati, sasa ipi ni miradi ya kimkakati na ipi ina maslahi ya Kitaifa? Wasiwasi wangu ni kwamba inaweza ikaongeza wigo wa misamaha. Waswahili wanasema wasiwasi ni akili! Ni wasiwasi wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile maamuzi ya Baraza la Mawaziri hayawezi kuombwa kwenye Kamati na hayawezi kuhojiwa kwenye Kamati, nilikuwa napendekeza kwamba basi Baraza la Mawaziri lifanye mapema maamuzi yake kabla ya mwaka wa fedha au bajeti ya mwaka unaokwenda haijapitishwa ili yale yaweze kuingizwa katika Jedwali la Misamaha ya Kodi wakati wa kujadili pamoja na Finance Bill, ili kusiwe na mgongano na kusiwe na matatizo yoyote. Lakini tukisema wakati bajeti inaendelea, halafu ndiyo Baraza la Mawaziri lifanye maamuzi ya kutoa misamaha ya kodi katika hiyo miradi ambayo itaonekana kimsingi ni ya kimkakati, itakuwa kwa kweli kidogo kuna matatizo kwa sababu Kamati haitaweza kuhoji wala Baraza la Mawaziri halitaweza kuhoji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilikuwa nashauri, ninakubaliana na mapendekezo ya Serikali, lakini nilikuwa nashauri tu kwamba maamuzi ya kusema miradi ipi isamehewe, itakayowezesha utekelezaji wa miradi ya kimkakati na kwa maslahi ya Taifa yafanywe mapema kabla ya mwaka wa fedha haujafika na yajadiliwe pamoja na Finance Bill.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, sina matatizo nayo, ushauri wangu ulikuwa ni huo. Nimalizie tena kukipongeza Chama changu cha Mapinduzi kwa ushindi tuliojizolea.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami napenda niungane na wajumbe wenzangu kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati ambao wamewasilisha taarifa zao katika Bunge letu asubuhi ya leo. Kwa kuwa muda wangu ni mfupi, napenda nijielekeze moja kwa moja katika masuala ambayo nimejipanga kuyachangia.

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza ni uvuvi. Eneo la uvuvi kwa kweli Serikali haijawekeza ipasavyo. Mara nyingi tumekuwa tukijielekeza kwenye operesheni zaidi kuliko kuwawezesha wavuvi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leseni za uvuvi zinafuata kalenda ya mwaka yaani Januari – Desemba. Januari ilivyoanza tu hata tarehe 15 bado operesheni za kuwasaka wasiokuwa na leseni zimeanza na kuwatoza faini kubwa zaidi ya shilingi milioni 1 kwa mvuvi mmoja wakati faini inaanza kutolewa baada ya mwezi Machi, kuanzia Januari, Februari mpaka Machi wanatakiwa wavuvi wakate leseni lakini mwaka huu kabla hata ya Februari operesheni imeanza, wavuvi wangu wa Naumbu, Msanga Mkuu, Mkubiru na Msimbati wamepigwa faini mpaka shilingi milioni 4, hali kwa kweli kule ni mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri pamoja na kwamba tumezungumza naye, walikuja wavuvi pamoja na Waheshimiwa Madiwani kutoka Kilwa, ameahidi kwenda Kilwa siku ya Jumapili. Nimuombe Mheshimiwa Waziri asiishie Kilwa Kivinje na Kilwa Masoko, katika ziara yake aende mpaka Mtwara, Msanga Mkuu, Mkubiru, Msimbati, Naumbu na Mgau kwa sababu kero hiyo kwa kweli ipo kwa wavuvi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutoa ushauri kwa Serikali, naomba wafanye utafiti wajue ni nyavu zipi zinazoweza kuvua dagaa na baada ya kuzijua Serikali yenyewe iingie mkataba na viwanda wanunue hizo nyavu, waweke mawakala wa kuuza hizo nyavu Kilwa, Mafia na Mtwara ili wavuvi wetu ikiwezekana wakopeshwe na wanaoweza wanunue ili kuondoa hii sintofahamu ya kila siku tunawaelekeza nyavu za kununua halafu baada ya siku mbili tunaenda kuzikamata hizo hizo tunazichoma moto. Kwa hiyo, niiombe Serikali yenyewe kama inavyofanya kwa pembejeo za kilimo na katika maeneo mengine na huku kwenye uvuvi yenyewe itafute mawakala wa kusambaza zana za uvuvi ambazo wao wamezipitia na kuzithibitisha na kuziona kwamba baada ya utafiti wao zinafaa kuvua dagaa, pweza na kamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo ulikuwa mchango wangu wa kwanza kwa kweli wavuvi wetu hawana amani lakini ni eneo ambalo kwa kweli kama Serikali hatuwawezeshi. Ukiacha mradi wa MANCEP ambao ulipita kipindi hicho, hakuna mradi mwingine wa uhakika ambao umekuja wa kuwawezesha wavuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nililetewa na Naibu Mheshimiwa Waziri injini ambazo kama Wizara iliona wangeweza kuzitoa kwa ruzuku kwa wavuvi. Nilivyoenda kuwatangazia wavuvi wangu waliniambia hizo mashine ni ndogo sana kwa kwenda nazo baharini. Sasa sijui wakati Wizara wananunua waliwashirikisha vipi wavuvi wetu.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo nilitaka nilichangie ni ununuzi wa korosho. Tulifurahi sana Serikali ilivyoamua kununua korosho kutoka kwa wakulima wetu na bei ambayo iliitoa lakini muda ambao tunauchukua katika mchakato mzima wa kununua korosho kwa kweli ni mrefu mno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kawaida ununuzi wa korosho unaanza mwezi Oktoba ikifika Desemba wale wanunuzi wanavyokwenda Chrismas inakuwa ni kama ununuzi umeishia, wanavyorudi sikukuu za mwaka mpya labda minada ikiendelea ni mitatu, minne na ununuzi unakuwa umeisha. Sasa hivi mpaka mwezi Februari hata asilimia 60 ya ununuzi haijafikiwa. Wamehakiki zaidi ya tani 200,000 lakini waliolipwa hawajafika hata tani 150,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha kushangaza katika takwimu zetu tunaambiwa katika vyama 605, wameshalipa vyama 600 lakini ukiangalia tani zilizouzwa hazijafika hata tani 150,000. Sasa sijui hizo takwimu zimekaaje, watatuambia wanaokuja kutujibia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine, Halmashauri zetu zote za Kusini ushuru wa korosho ndiyo chanzo chetu kikubwa cha mapato. Mpaka sasa hivi tunavyozungumza mwaka wa fedha 2018/2019 bado miezi mitano tumalize na hatujapata ushuru na hatuna uhakika kama tutapata na hatujui kama tutapata tunaupata lini. Niiombe Serikali suala la ushuru kama ambavyo wadau wengine wamelipwa na kwa kawaida ileile Sh.3,300 ambayo Serikali ilisema itanunua kutoka kwa wakulima, wadau wote wangepata pesa zao kutoka kwenye pesa zilezile bila hata kuhitaji bajeti nyingine.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali ijitahidi kuhakikisha wadau wote wanaohusika katika ununuzi wa korosho na wakulima wetu hasa wakubwa maana yake wakulima wakubwa mpaka sasa hivi hawajaanza kulipwa. Imekuwa kama ni adhabu sasa kuwa mkulima mkubwa wa korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Maji na pia nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya. Nianze kwa kuipongeza Wizara nikianza kumpongeza Waziri, Naibu wake, Katibu Mkuu pamoja na watendaji kwa kazi ambayo wanaifanya. Ninaimani kabisa kwamba wakiwezesha pesa za kutosha wataweza kufanyakazi nzuri zaidi kuliko ambavyo sasa hivi wanafanya.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi zangu hizo, ningependa kuchangia maeneo mbalimbali yanayogusa katika eneo langu. Kwanza nianze na ule Mradi wa Maji kutoka Mto Ruvuma kupeleka Mtwara Mjini. Mradi ule ukitekelezwa utapeleka maji katika vijiji vya Mtwara Vijijini zaidi ya 30, lakini mpaka sasa hivi mradi huu umekuwa ukisuasua. Ukikutana na watendaji wanakwambia mradi upo, wakati mwingine ukikutana na Waziri anasema huu mradi haupo. Kwahiyo ningependa Waziri atakapokuja kutoa majibu atuambie Mradi huu waKutoa Maji Mto Ruvuma upo au haupo na kama haupo sisi wa Mtwara Vijijini vile vijiji ambavyo vilipangiwa kupata maji kutoka katika mradi huu vitapelekewa maji kwa mradi gani?

Mheshimiwa Spika, katika kupitia bajeti nimekuta sehemu imeandikwa kwamba mradi wa kutoa maji mto Ruvuma kupeleka Mtwara kwa gharama ya shilingi bilioni moja. Kwa kweli imenitia wasiwasi hivi kweli unaweza ukatoa maji Mto Ruvuma ukafikisha Mtwara Mjini kwa shilingi bilioni moja au hii ni token tu kama mradi utakuwepo wataongezea pesa au bado wako katika kusuasua uwepo au usiwepo. Kwahiyo Mheshimiwa Waziri atupe ufafanuzi.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo pia nataka ufafanuzi ni suala la mradi wa maji katika Mji wa Mtwara na Babati, yenyewe imetengewa Sh.2,500,000,000 kwa kweli kwa miji miwili na Mheshimiwa Waziri ametembelea katika Mradi wa Mtwara nilikuwepo, ameona changamoto zilizopo, maji yanayokwenda katika Mji wa Mtwara zaidi ya kuyatibu hayachunjwi, yanakwenda na rangi yake ileile. Mheshimiwa Waziri kazi ni kubwa inayotakiwa kufanyika pale.

Mheshimiwa Spika,tunayomiradi ya maji ambayo ni mibovu, tunao Mradi wa Kitere, ambao unatakiwa upeleke maji katika Vijiji vya Chemchem,Nakada, Chekelenina Lilido, lakini mradi huu ulijengwa muda mrefu na sasa hivi unahitaji ukarabati mkubwa, lakini nimeangalia kwenye hii bajeti sijaona. Tunao Mradi waMbuo – Mkunwa,Mradi huu unaitwa Mbuo- Mkunwa lakini Mkunwa hata hayo maji hawajayaona, upanuzi kila siku utafanyika, utafanyika. Mradi huu tumewapa MTUWASA lakini pamoja na kuwapa MTUWASA hatuoni kasi wala manufaa ya kuwapa wao, tulitegemea baada ya wao kupewa huu mradi, basi vijiji vyote vinavyotakiwa kuhudumiwa na mradi huu wangekuwa wameshafikiwa.

Mheshimiwa Spika,nimpongeze na nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa Mradi wa Lyowa kwasababu amenihakikishia kwamba pesa zimeingia, nami nitafuatilia kujiridhisha kama pesa ya kununua pump imekwenda ili mradi huu uweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika,tunayo changamoto ya upatikanaji wa maji ya uhakika katika Mradi wa Mbawala Chini, ambao wenyewe unatakiwa kuwahudumia wananchi wa Manispaa ya Mtwara, Mbawala lakini na Kata ya Nanguruwe na wenyewe mara nyingi umekuwa unapata uharibifu wa mitambo, lakini hata usambazaji wake na wenyewe haujafikia kiwango ambacho kinahitajika.

Mheshimiwa Spika,tunazo kata ambazo kwa kweli zinachangamoto ya upatikanaji wa maji kwa kiasi kikubwa, Kata ya Lipwidi, Kata ya Mangopachanne, Kata ya Madimba na Kata ya Tangazo tunao mradi, lakini kuna vijiji ambavyo bado havijafikiwa na mradi huu. Nimwombe Mheshimiwa Waziri nimeangalia kwenye bajeti kuna miji kuna miradi, nimesoma, nimeangalia katika mkoa wangu, naona Mradi wa Makonde, nimeuona Mradi wa Mangaka nimeiona miradi mingi, lakini mradi haswa wa kuhudumia Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara nimejaribu kuutafuta mradi hasa wa kusema huu ndiyo utasaidia kuondosha kero ya maji katika Halmashauri ya Mtwara Vijijini sijauona.

Mheshimiwa Spika,Mheshimiwa Waziri alipotembelea Mkoa wa Mtwara aliuona Mradi wa Maji wa Msanga Mkuu, aliona changamoto ya maji kubadilika rangi, ambapo hata wananchi wanaogopa kunywa maji yale kutokana na rangi na alituahidi kwamba angeleta pesa za kuwezesha mradi ule ili lijengwe chujio dogo la kuweza kusafisha yale maji. Nimejaribu kuangalia humu sioni chochote.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo nataka kulizungumza, inaonesha Wizara baadhi ya Halmashauri au Mikoa hawajui ilivyokaa au ikoje. Nimeangalia ukurasa wa 163, nikaangalia pesa ambazo zimeenda kwenye mikoa kwenye miradi mbalimbali, nimesikitika kuona kwamba wilaya yangu kwa Wizara ya Maji inaonesha kwamba wamenitengea pesa nyingi, lakini kiuhalisia hizo pesa haziji kwenye wilaya yangu. Inaonesha wilaya yangu nimetengewa shilingi milioni 943 ambapo shilingi milioni 20 zinaenda Kilambo, milioni 70 zinakwenda Msanga Mkuu, milioni 93 zinaenda Nanyamba - Malanje na milioni 630 zinaenda Mradi wa Maji wa Ujenzi wa Chipango, Namyomyo, Manyuli,Mnavirana Mkaliwata. Hivi vijiji huu mradi ni wa Wilaya ya Masasi DC, zaidi ya shilingi milioni 630.

Mheshimiwa Spika, sasa huko wakikaa wanaonesha kwamba milioni 600 imeenda Mtwara DC, kuna milioni 128 ambazo ni za maji Nanyamba - Mbembaleo. Kwahiyo kiuhalisia Mtwara Vijijini imepata milioni 90 peke yake, lakini hapa inaonesha zaidi ya milioni 900 imeenda Mtwara Vijijini.Hii si haki na naomba hizo pesa ambazo zinaonesha milioni 600 zimekwenda Mtwara Vijijini wakati zimeenda Wilaya ya Masasi, basi watafute popote zinapopatikana ziweze kuja Mtwara vijijini ili tuweze kuondoa changamoto. Kwa sababu Masasi kama Masasi wamewatengea pesa zao, tena nyingi bilioni 1.8, halafu wakachukua milioni 600 badala ya kupeleka Masasi ikaonesha wamewapa bilioni 200 na nukta zake kule wamekuja kuziweka Mtwara Vijijini, kama zilikuwa zinafichwa sijui, lakini sidhani kama ni kwa bahati mbaya. Naomba hizo milioni 600 nilizokuwa nimetengewa zije zote Mtwara Vijijini na Masasi wawawekee kwamba wamewapelekea bilioni 200.

Mheshimiwa Spika, napenda nirudie tena kuwaomba, wakati wa kuandaa hizi bajeti na takwimu zetu na vijiji tujiridhishe, kwasababu nitaonekana mlalamishi, nimeletewa milioni 900, wakati kiuhalisia nimeletewa milioni 90. Nisikitike sana kwa hilo na nimwombe Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa majibu anijibu pesa hizo ambazo zilistahili kwenda Mtwara Vijijini zitapelekwa lini na miradi ya Mtwara Vijijini itatekelezwa vipi?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi nashukuru kwa kunipa dakika tano nitajaribu kukimbia kimbia.

Mheshimiwa Spika, ahsante niipongeze Wizara kwa kazi kubwa wanaoifanya katika kuhakikisha kwamba miundombinu ya nchi yetu inaboreshwa.

Mheshimiwa Spika, naomba nianzie jimboni kwangu ambako kwanza ningependa suala la barabara ya Mtwara - Msimbati - Madimba - Kilambo ambazo ni barabara zinazounganisha nchi yaani Tanzania na Mozambique ambayo ni sera yetu kuhakikisha kwamba barabara zinazounganisha nchi zinajengwa kwa kiwango cha lami, Mheshimiwa Waziri naomba utakapokuja kunijibu basi uniambie imefikia wapi suala la kujenga barabara ya Mtwara - Msimbati - Madimba - Kilambo kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, pia kuna suala la barabara ya kutoka Hiari -Nanguruwe ambayo ni mchepuko, sasa hivi kutokana na kiwanda cha saruji ambacho ni kikubwa sana magari yote yanayokwenda Newala hayapiti tena Mtwara yanatumia barabara hii tumeiomba Serikali, nimekuja kwako Mheshimiwa Waziri nimezungumza na Meneja wa TANROADS kuomba barabara hii ichukuliwe na Wizara kwa sababu inapitisha malori makubwa ambapo TARURA peke yake hawawezi kuijenga barabara hii ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri yangu tulikuwa tunajenga barabara kwa kiwango cha lami kutoka Kivukoni pale Msemo kwenda Msanga Mkuu, lakini barabara hii imekuwa na changamoto kubwa sana watu wa bandari wa Mtwara hawataki barabara ipite katika maeneo yao, sasa maeneo yote hata Dar es Salaam kuna barabara ambazo zinapita ndani ya eneo ya bandari na kule Msanga Mkuu ni lazima upite katika bandari ndipo uweze kufika katika vijiji vyetu.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri aingilie kati kwa sababu barabara hii ilikuwa inajengwa sasa hivi imesimama kwa eti tu kwamba hatuwezi kujenga barabara ya lami kupita eneo la bandari eneo ambalo hata kuendelezwa bado alijaendelezwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba uingilie kati suala hilo.

Mheshimiwa Spika, tunayo barabara yetu ya kutoka Mpapura kwenda Kitere mpaka Mkwichi kule Mtama, naomba hii barabara inaunganisha mikoa, Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Mtwara kama kawaida tunaomba barabara hii ijengwe kwa kiwango cha lami kwa sababu ndiyo sera kuziunganisha kwa kiwango cha lami barabara zote ambazo zinaunganisha mikoa.

Mheshimiwa Spika, na mimi niungane na wenzangu kuzungumzia suala la Bandari ya Bagamoyo, hata wenzetu China walivyotaka kuendeleza nchi yao, walivyotaka kuanzisha maeneo ya special economic zone walianzia na China ya Mashariki ambako ndiko ambako wanapakana na bahari. Sasa kuanzia Djibouti mpaka tunafika kule South Africa, sisi hapa tulikuwa na nafasi kubwa sana ya kuwa na bandari kubwa ambayo itachukuwa meli za four generation ambazo zingeweza kuleta mizigo baada ya kufika pale ile mizigo sasa ndiyo ikawa inaenda kwenye bandari zingine za Beira, Mombasa, Dar es Salaam na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali yetu suala hili waliangalie kwa mtizamo mpana zaidi na hasa wakisikiliza na Wabunge michango yao pamoja na mchango wako.

Mheshimiwa Spika, na suala la mwisho ni suala la Reli kutoka Mtwara kwenda Mbambabay na matawi la kwenda Liganga na Mchuchuma. Tunategemea kuchimba chuma, kuchimba makaa ya mawe na alivyokuja Waziri wa Ujenzi alisema kuna tender ya kupeleka...

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa juhudi kubwa sana anazozifanya katika kuhakikisha kwamba tunaingia katika uchumi wa viwanda na tunakua kibiashara na tunaweka mazingira mazuri ya biashara. Niiombe Wizara ya Viwanda na Biashara na Serikali kwa ujumla, tupunguze muda wa majadiliano pale ambapo tunapata wawekezaji katika miradi yetu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti wakati napitia wakati napitia kitabu cha hotuba ya bajeti malengo ya karibu kila idara, nilikuwa naangalia NDC, kila unapoangalia ni kuendelea na majadiliano. Nimechanganyikiwa zaidi pale ambapo nimekuja kuangalia Mradi wa Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya bajeti ya mwaka jana walikuwa wameshafika eneo nzuri kabisa ambako mwaka huu nilikuwa na matumaini kwamba labda mradi tungeambiwa sasa hivi unakaribia kutekelezwa. Nilichokiona katika kitabu cha hotuba ni kwamba baada ya kuwa tumepitisha ile Sheria ya Kulinda Maliasili zetu inayonyesha majadiliano ya Liganga na Mchuchuma yameanza upya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaenda mbele, tunarudi nyuma. Kwa kweli inasikitisha sana, kama majadiliano haya yangekuwa yamekwisha kwa wakati, nina uhakika kabisa SGR hii inayojengwa tungejenga kwa kutumia chuma cha Liganga na Mchuchuma badala ya chuma ya kutoka Japan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao Mradi wa Reli kutoka Mtwara kwenda Mbambabay na matawi kwenda Liganga na Mchuchuma. Wawekezaji wengi sana wameonyesha nia ya kujenga reli hii kwa njia ya PPP lakini wote wanavutiwa na makaa ya mawe na chuma iliyoko Liganga na Mchuchuma. Kama majadiliano hayataisha watafanya wale ambao wanahamu ya kujenga reli hii waondoshe ile hamu yao kwa sababu kila siku ni kujandiliana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, NDC watuambie wamekwama wapi kwenye Mradi wa Liganga na Mchuchuma. Mimi nakusudia kutoa shilingi kwa sababu mradi huu ukiendelea ndiyo utaifanya Bandari ya Mtwara ifanye kazi vizuri zaidi na hata Mji wa Mtwara uwe wa viwanda kwa sababu hiyo chuma na makaa ya mawe yatawezesha SEZ au EPZA ya Mtwara kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majadiliano yanaendelea ya Kiwanda cha Mbolea kule Msanga Mkuu, huu unaingia zaidi ya mwaka wa sita majadiliano yanaendelea. Mimi napenda kujua au Waziri wa Viwanda na Biashara au Waziri wa Fedha wakija watuambie hivi wenzetu Rwanda wao wanajadiliana kwa kwa stahili ipi ambapo anaweza akaja mwekezaji ndani ya siku tatu wameshamaliza kujandiliana, wameshakubaliana, wameshasaini mikataba na sisi haswa hicho tunachokwama ni kitu gani? Au hao wanaojadiliana wanalipwa vizuri sana, kwa hiyo, majadiliano wamefanya ni sehemu ya maisha? Hebu tuangalie suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie eneo la biashara, siyo siri sasa hivi Kariakoo kumekufa. Kariako ilikuwa inapokea wafanyabiashara kutoka Congo, Zambia, Malawi, Zimbambwe mpaka Uganda, sasa hivi Watanzania tunaenda Uganda kununua bidhaa ambazo zimepita katika bandari yetu. Niiombe Serikali iangalie kuna nini kinachoua Kariakoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo siri ukienda Kariakoo maduka mengi yamefungwa na hata ukitaka banda leo Kariakoo unapata wakati zamani kupata banda Kariakoo ilikuwa ni shida. Sasa kama Serikali tujiulize ni nini kimewakimbiza majirani zetu kuja kufanya biashara Kariakoo kwa sababu Karikaoo ilikuwa ndiyo Dubai ya Afrika Mashariki na Afrika ya Kati. Ni kitu gani sasa kinachowafanya watu waende Uganda wakimbie Kariakoo? Namuomba Waziri wa Viwanda na Biashara alifanyie kazi suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine ni vizuri tu Serikali ikapokea ushauri kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge. Kama tutakumbuka wakati tunapitisha Sheria ya Manunuzi, Kamati ya Bajeti ilikuja na mapendekezo ya kuweka kipengele cha kutumia force account kwenye miradi yetu, kwenye Kamati Serikali ililikataa pendekezo hilo na Kamati ikalazimika kuja kulileta pendekezo ndani ya Bunge na bahati nzuri pendekezo lilipita. Sasa hivi force account ndiyo inayotuwezesha kujenga vituo vya afya, hospitali zetu na miradi mingi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa lakini ilipita kwa kutumia nguvu za ziada hapa na sasa hivi tumesahau ilipitapitaje lakini manufaa makubwa tunayapata kwa kwa kutumia force account ambayo ilipita kwa shida sana ndani ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna taasisi na kodi nyingi katika biashara zetu. Sasa hivi ukiwa na kampuni yako unatakiwa ulipe PAYE, Workers Compensation na SDL, kwa nini hii kitu isije ikalipwa kwa wakati mmoja? Sasa hivi ukishalipa PAYE atakuja mtu wa Workers Compensation kwa wakati wake, atakuja mtu wa SDL kwa wakati wake, atakuja OSHA kwa wakati wake, atakuja TFDA kwa wakati wake, yaani unasikia pressure inapanda na kichwa kinauma. Kwa nini wasije kwa wakati mmoja halafu unalipa wenyewe wakaenda kugawana huko kwa sababu kila mtu chake kinajulikana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo ndiyo vinavyokwamisha biashara zetu na pia ndivyo vinavyokwamisha uwekezaji katika nchi yetu, ni ugumu katika ufanywaji wa biashara. Hata kuandika tu zile return za VAT kwa wakati wake, SDL kwa wakati wake, PAYE kwa wakati wake, Workers Compensation kwa wakati wake, navyo vinachosha na vinatia ugumu katika kufanya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja lakini lile la Liganga na Mchuchuma lenyewe tutalijua kesho, ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.Napenda nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili niweze kuchangia mpango wa maendeleo kwa mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuipongeza Serikali kwa utekelezaji mzuri wa mpango ambao unaendelea. Tumeona upanuzi waBandari zetu zote kuanzia Mtwara, Dar es salaam na hata Tanga. Nina imani kabisa upanuzi wa bandari hizi utawezesha kwa kiasi kikubwa utekelezaji wa Serikali ya viwanda, kwasababu matarajio yetu bandari hizi zitaweza kubeba malighafi na pia kubeba bidhaa ambazo zinazalishwa katika maeneo yetu.Sasa hivi Bandari yetu ya Mtwara inatumika kusafirisha saruji kupeleka Comoro, kupeleka Zanzibar lakini ni imani yangu kwamba Bandari yetu ya Mtwara itakapokamilika, upanuzi ule ambao unaendelea utawezesha ubebaji wa korosho kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tulikuwa na korosho ambayo ilikuwa haijapata wanunuzi. Baada ya kupata wanunuzi, meli zinazokuja sasa hivi za kizazi cha nne(fourth generation), meli moja tu ikija ku-park basi nyingine zinasubiri kwa muda mrefu. Ndiyo kusema ule muda ambao meli inachukua kusubiria ili nyingine itoke ili nyingine ije i-park pia inaathari katika bei ya korosho kwasababu mnunuzi anawekewa na ile gharama ya kusubiria. Ni imani yetu kwamba mara baada ya upanuzi wa Bandari ya Mtwara utakapokamilika meli nyingi zaidi zitaweza ku-park kwa wakati mmoja na kuweza kuchukua korosho kwa wakati mmoja na hivyo kupunguza gharama za uendeshaji na faida ile itakwenda moja kwa moja kwa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuiomba Serikali yetu; upanuzi waBandari ya Mtwara uende sambamba na ujenzi wa reli ambao umeshafikia hatua nzuri kwa maana ya upembuzi yakinifu umekamilika, tathmini ya gharama za fidia nao umekamilika. Kwahiyo, tulikuwa tunaomba ili Bandari ile ya Mtwara iweze kufanyakazi vizuri, basi ule ujenzi wa reli ya kutoka Mtwara kwenda Mbambabay na matawi yake ambayo yanakwenda Liganga na Mchuchuma sambamba na miradi ya Liganga na Mchuchuma kwa maana ya chuma na makaa ya mawe na yenyewe sasa ianze kutekelezwa ili bandari pamoja na reli viweze kufanyakazi kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Mpango wetu tunaonesha tuna nguvukazi ya kutosha yaani watoto wenye umri wa miaka 0-14 lakini pia hata kwenda kwenye miaka 45 ambayo ndiyo nguvukazi kubwa tunayoitegemea ni zaidi ya asimilia 50. Nguvukazi ile kwa maana ya watoto wenye umri ule wa miaka 15, 14 mpaka miaka 30 ili tuweze kunufaika nayo na iweze kutumika vizuri katika kukuza uchumi ni vizuri tukawekeza katika rasilimali watu na uwekezaji wa rasilimali watu ili uweze kuwa na manufaa zaidi ni lazima tuanze kuwekeza katika mwaka sifuri mpaka siku zile1,000za mwanzo nikimaanisha lishe kwa watoto wetu. Kama tutawekeza kwa maana ya lishe ya watoto kuanzia siku sifuri kwa maana ya ujauzito mpaka anafikia siku 1,000 zile ndipo hapo tutakapowapeleka shuleni na hata kwenye vyuo tutaweza kupata matunda mazuri sana na yataweza kusaidia katika kukuza uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumzia lishe watu wengine wanakuwa hawaelewi, lakini zile siku 1,000 tangu mtoto akiwa kwenye tumbo la mama yake mpaka anazaliwa na siku zile 1,000 ndizo zinazojenga ubongo wa mtoto na ndizo zinazoweza kumfanya aweze kujadiliana vizuri, aweze kushika vizuri masomo darasani na hivyo hivyo aje kuchangia katika uchumi wa nchi. Nchi kama Japan hazina rasilimali kama ambazo sisi tunazo, lakini wenzetu wamewekeza katika rasilimali watu, wamewekeza katika vichwa vya vijana wao, ndiyo maana wanaweza kutengeneza magari, wanatengeneza computer na wameweza kuendeleza nchi zao kwasababu wamewekeza katika rasilimali watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo nataka pia nilisisitize; tuache mtazamo wa kuwekeza zaidi kwenye vyuo vikuu na tukaacha hizi taaluma za kati kwa maana mafundi Mchundo, kwa maana vyuo vyetu vile ambavyo vinawajengea uwezo zaidi kuliko vyuo vikuu.Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana atakuwa shahidi, sasa hivi wanaomba vibali vya kufanyakazi katika nchi yetu ni katika nafasi za fundi mchundo zaidi kuliko hata wahandisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na mkutano wa wadau wiki iliyopita kule Mtwara, mkutano wa uwekezaji na katika makundi yaliyopangwa kwenda kutembelea mimi nilikwenda kutembelea kiwanda cha Dangote. Tumekuta pale wanajenga mtambo ambao utazalisha umeme kwa kutumia makaaya mawe, kutumia gesi, kutumia mafuta yaani mtambo uko combined kwa pamoja yaani mafundi mchundo waliojazana pale ni shemeji zangu kutoka India ndiyo waliojazana kwa maana kwamba sisi hatuna, tuna wahandisi lakini hatuna ma-technician kwahiyo tunalazimika sasa kuagiza kutoka nje. Kwahiyo, naomba tuwekeze katika vyuo vyetu vya ufundi, tuwekeze katika VETA zetu,kwasababu kama tunavyofahamu Injinia mmoja anahitaji zaidi mafundi mchundo zaidi ya watano na kuendelea. Baadhi ya vyuo vyetu vyote ambavyo vilikuwa vinatoa mafunzo hayo sasa hivi vyote tumevigeuza kuwa vyuo vikuu. Sasa hii rasilimali watu tuliyonayo ambayo ni mtaji mkubwa sana katika ukuzaji wa uchumi. Ni lazima tuwekeze kwa kiasi kikubwa ili tuweze kuitumia inavyopaswa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo tunaweza tukalitumia katika kukuza uchumi wetu ni katika eneo la uvuvi; niiombe sana Serikali yangu iwekeze kwenye uvuvi. Iwasaidie wavuvi kupata zana bora za kisasa ambazo wanaweza wakazitumia. Kwenye uvuvi tofauti na kilimo unahitaji kulima, unahitaji pembejeo, unahitaji mbolea; kule baharini ni kwenda kuvuna tu. Tunachotakiwa kupata ni zana za kisasa ambazo zitatuwezesha kwenda katika bahari kuu na kuweza kuvuna rasilimali ambazo Mwenyezi Mungu ametujaalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi wavuvi wetu ni kama aneo ambalo limesahauliwa. Ukienda Msimbati, nenda Nalingu, nenda Msanga Mkuu tunachokifahamu Serikali ni kwenda kufanya operation lakini zile operation zinatokana na kwamba hawana hizo zana bora. Hatujawapa kama ambavyo wakulima au wafugaji tunawapa pembejeo, tunawasaidia kuwajengea majosho, tunawasaidia kuwaunganisha katika vikundi na kuwawezesha.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hawa malizia.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kuomba wenzetu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, wawawezeshe zana na ujuzi wavuvi katika eneo hilo tunaweza kupunguza umaskini kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika taarifa ambazo zimewasilishwa kuhusu TAMISEMI, Utawala Bora. Nami napenda kujielekeza zaidi kwenye taarifa ya TAMISEMI na Utawala Bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa ushindi mkubwa ambao tumeupata katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambao haujawahi kutokea. Nina uhakika kabisa kwamba Uchaguzi Mkuu tutashinda kwa asilimia nadhani zile zile au zaidi ya pale. Kinachofanya chama kushinda siyo Tume Huru, ni maandalizi ya Chama na jinsi gani chama kinakubalika ndani ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge tuliomo humu ndani tumeshinda kupitia Wakurugenzi hao hao ambao leo tunawaona hawafai. Kwa hiyo, mimi naomba tu tujiandae kwa uchaguzi wa mwaka 2020 kwa Tume yetu ile ile ambayo ndiyo imewaingiza humu ndani ya Bunge na nina uhakika wale wenye sifa watashinda na wale wengine ndio hivyo tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kuipongeza TAMISEMI kwa jinsi ilivyosimamia ujenzi wa Hospitali za Wilaya pamoja na Vituo vya Afya kupitia force account. Gharama ambazo tumezitumia kujenga hospitali moja kwa tulivyozoea nadhani hata robo ya hospitali isingeweza kufikiwa. Naishukuru TAMISEMI kwamba tumepata hospitali ya Wilaya, Vituo vya Afya huko Kilambo, Mahurunga kimekarabatiwa, Mkunwa kinaendelea kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunayo maombi ambayo yako TAMISEMI ya Kituo cha Afya Mango Pachanne na pia kutokea Msimbati, Madimba, Ziwani, Nalingu mpaka Msangamkuu tunahitaji kupata Kituo cha Afya kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kuamua kutupatia zaidi ya shilingi bilioni 15 kumalizia Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini. Sikupata nafasi kuchangia Wizara ya Afya, nachukua fursa hii kuishukuru sana Wizara ya Afya kwa jinsi inavyosimamia ujenzi ule kupitia National Housing. Nina imani kabisa baada ya mwaka mmoja Mtwara kwa maana ya Mkoa Kanda ya Kusini, Wilaya zetu zitakuwa zimeboresha kwa kiasi kikubwa huduma za afya. Ndiyo maana nasema sina wasiwasi hata kidogo kwamba tutashinda kwa kishindo katika Uchaguzi Mkuu unaokuja, kwa sababu Serikali ya Chama cha Mapinduzi imetekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, imetatua kero za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza tena Serikali kwa kutoa mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Kwa kweli imekuwa ni chachu na imeweza sana kuongezea mitaji wanawake wetu, vijana wetu pamoja na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kutoa mapendekezo kidogo kwa upande wa wenzetu wenye ulemavu hasa maeneo ya vijijini. Tunasema ili wawe na kikundi, wanahitajika wawe angalau 10. Kijiji kingine unakuta labda walemavu wako watatu, wanne kwa hiyo, inakuwa ni ngumu hasa ukizingatia wao ni walemavu. Kwa hiyo, hawezi yeye akasema aungane na mlemavu labda wa Kata nyingine au wa Tarafa nyingine na mara nyingi kikundi ni lazima muwe ni watu mnaofahamiana, mnaoleweana. Kwa hiyo, nawaomba wenzetu TAMISEMI waingalie hiyo Kanuni ili waweze kuirekebisha iweze kupunguza idadi ya wanakikundi hasa kwa wenzetu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA naiomba Serikali iongeze kiwango ambacho TARURA wanapewa kwa ajili ya ujenzi wa barabara. Asilimia 30 wanayoipata kwa kweli ukilinganisha na mtandao wa barabara ambao uko katika maeneo yao ni kidogo sana. Kwa hiyo, tunaomba waongeze kama haiwezekani 50 kwa 50, basi angalau asilimia 40. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na ninarudia tena kusema tutashinda Chama cha Mapinduzi kwa kishindo kikubwa sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kupata fursa ya kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya. Nadhani sifa ambazo wanapewa kwa kweli wanastahili sana; si wachapakazi tu lakini pia ni wasikivu, wanyenyekevu na wanashaurika, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda wangu ni mchache, naomba niende moja kwa moja katika maeneo ya Jimbo langu. Nishukuru sana kwamba vijiji vingi katika Jimbo langu vimepata umeme lakini nina kata mbili; Kata ya Muungano na Kata ya Moma hazina hata kijiji kimoja ambacho kina umeme. Nikushukuru Mheshimiwa Waziri juzi ulivyokuja umeniahidi vijiji viwili katika Kata ya Muungano na Vijiji viwili katika Kata ya Moma, nakushukuru sana na pia umeniahidi umeme katika Sekondari ya Nanguruwe. Pia niombe umeme katika sekondari yangu ya Lilido na yenyewe Mheshimiwa Waziri nayo niweze kupata umeme ili wanafunzi wangu waendelee kufanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nikupongeze sana kwa kuanzisha mpango wa kupeleka gesi ya majumbani. Mwaka jana tulifanya uzinduzi pale katika Sekondari ya Mtwara kwa sababu sasa hivi inachukua na wasichana, Sekondari ya Ufundi Mtwara lakini mradi ule naona kama unaenda taratibu na nilivyosoma katika kitabu chako cha hotuba naona kwamba bado mko katika usanifu. Nikuombe Mheshimiwa Waziri huo usanifu uharakishwe ili mradi ule uanze kutekelezwa kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, eneo ambalo ningependa kulisisitiza ni suala la utoaji wa leseni za utafutaji na uendelezaji wa gesi. Mheshimiwa Waziri nimeshakuja kwako zaidi ya mara mbili na Kampuni ya Ndovu Resource wakiomba leseni kwa ajili ya kuendelea kutafuta gesi na pia wakiomba leseni kwa ajili ya kuendeleza maeneo yale ambayo tayari gesi imepatikana, huu unaingia mwaka wa pili. Mheshimiwa Waziri nikuombe chondechonde tunasema kwa Kimakonde hivi vibali au hizi leseni kwa nini zinachukua muda mrefu hivi? Mji wa Mtwara sasa hivi unasinzia, kipindi kile wakati utafutaji unaendelea, mji ulichangamka na uchumi ulikuwa unakua.

Mheshimiwa Spika, tukuombe hayo majadiliano yakamilike, mnachojadiliana ili leseni zitolewe kwa watafutaji wa gesi na wale ambao tayari wameshapata gesi wanataka kuendeleza vitalu vyao haswa hao watu wa Ndovu Resource wamechimba katika Jimbo langu wamegundua zaidi ya maeneo matatu, sasa wanaomba leseni ya kutaka kuendeleza shughuli tangu mwaka 2017 mwezi wa kumi wameleta maombi mpaka leo bado majadiliano naambiwa sijui mkataba upo kwa AG.

Mheshimiwa Spika, nakusudia kutoa shilingi ili niambiwe ni lini leseni zitatolewa kwa watafutaji na waendelezaji wa gesi kwenye vile vitalu vyao. Mheshimiwa Kalemani tangu umeingia hujatoa leseni hata moja na watu wapo wanaotaka kutafuta hiyo gesi, wapo wanaotaka kuendeleza hizo gesi lakini leseni imekuwa ni mtihani.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa AG bahati nzuri upo, utasaidia katika kurudisha hiyo shilingi ya Mheshimiwa Waziri kwa sababu Waziri hastahili hata kidogo kunyang’anywa shilingi lakini naambiwa mambo yote yapo kwako lakini ili nifike kwako ni lazima nipitie kwa Waziri. Kwa hiyo, nitachukua shilingi ya Waziri ili Mheshimiwa AG ufanye kazi kwa haraka ya kumuwezesha Waziri kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo nilitaka nalo nipate ufafanuzi ni kuhusu Kiwanda cha Mbolea cha Msanga Mkuu kupitia Kampuni ya HELM…

SPIKA: Bahati mbaya dakika tano zimeisha.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kuunga mkono hoja lakini Msanga Mkuu na suala la leseni nipate majibu. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti yetu ya mwaka 2019/2020. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema ya kuweza kusimama katika Bunge hili. Nichukue fursa hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wao ambao wameshiriki kwa namna moja au nyingine katika kuandaa mpango na bajeti ya mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti yetu imeangalia utekelezaji wa Chama chetu cha Mapinduzi, imengalia Mpango wa Miaka Mitano kuanzia 2016-2021 na pia umeangalia kero za wananchi na misingi ya kukuza uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niipongeze Serikali kwa kuendeleza ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge, kwani ujenzi wa reli ni miongoni mwa vipaumbele katika mpango wetu wa miaka mitano, mpango wa maendeleo ambapo katika mpango wetu wa maendeleo tulisema kabisa uendelezaji wa miundombinu na ukarabati ni suala muhimu sana kwa maendeleo endelevu ya uchumi wetu. Kama tunavyofahamu reli ndiyo usafiri rahisi sana wa mizigo na hata abiria kushinda usafiri mwingine wa aina yoyote ile. Kwa hiyo sina budi kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kuhakikisha kwamba hili suala la standard gauge linajengwa na linakamilika.

Pia nipongeze kwamba mchakato wa kujenga reli ya kutoka Mtwara mpaka Liganga na Mchuchuma uko katika hatua nzuri, upembuzi yakinifu umeshafanyika na nimeona katika mpango na bajeti kwamba, mchakato unaendelea vizuri. Kwa hiyo mimi naipongeza sana Serikali kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naangalia katika bajeti ya upande wa pili, mapendekezo wanasema kwamba bajeti iangalie maendeleo ya watu na siyo maendeleo ya vitu. Unapozungumzia reli, unapozungumzia barabara, unapozungumzia standard gauge, yote hayo ni vitu vinavyolenga maendeleo ya watu. Huwezi kutenganisha maendeleo ya watu na vitu, utakuzaje uchumi kama usafiri wako si wa uhakika. Kama hauna umeme wa uhakika, maendeleo ya watu unayafikiaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nikasema kwenye mpango wa maendeleo wa miaka mitano kipaumbele cha kwanza kilikuwa ni kuhakikisha tunapata umeme wa uhakika. Umeme wa uhakika ndiyo utakaowezesha maendeleo ya viwanda, umeme wa uhakika ndiyo utakaohakikisha kwamba kilimo chetu kinakuwa bora na kinakuwa kwa sababu utaruhusu usindikaji wa mazao katika viwanda vyetu na ndiyo utakaoruhusu kilimo cha umwagiliaji, kusuma pump za kusukuma maji. Sasa ni lazima uwe na pa kuanzia, pa kuanzia ni kuhakikisha kwamba una miundombinu muhimu ya kuhakikisha uchumi wako unakuwa, ndipo hapo watu watakapokuja kuingia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hakuna umeme wa uhakika ina maana viwanda havitafanya kazi kwa uhakika, hakuna watu watakaowekeza kwenye viwanda na kama watu hawatawekeza kwenye viwanda ajira hizo unazitoa wapi. Kwa hiyo maendeleo ya watu na vitu vinakwenda kwa pamoja, lakini unaanza kuboresha miundombinu, kuhakikisha una umeme wa uhakika, ukiwa na umeme wa uhakika mambo mengine yatajipa yenyewe. Ajira zitakuja, maisha ya watu yataboreka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi niipongeze sana Serikali kwa kuhakikisha tunakuwa na umeme wa uhakika. Katika Mpango wa Miaka Mitano tuliridhia kwamba kipaumbele chetu namba moja ni kuhakikisha tunapata nishati ya umeme ya gharama nafuu na ya uhakika. Sasa inapatikana katika chanzo kipi nadhani hilo ni suala la watendaji na Serikali. Sio mtu umwambie wewe ni golikipa, halafu umwambie uangukie kushoto na usidakie upande wa kulia, hizo si kazi zetu. Sisi tunachopaswa ni kuridhia ile mipango.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze Serikali kwa kuendeleza bandari zetu ikiwemo Bandari ya Dar es Salaam, Bandari ya Tanga na Bandari ya Mtwara. Kazi inayofanyika katika kuzipanua bandari zetu hizi itaifanya nchi yetu kuwa lango kuu la kibiashara ambapo tutaweza kufanya biashara na nchi ambazo hazina bandari au hazina bahari. Kwa hiyo, itakuza uchumi wetu, itapunguza gharama za usafiri na itatufanya pia kuwa kitovu cha kibiashara na tutaweka mazingira mazuri ya kibiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze Serikali katika suala zima la kujenga na kukarabati viwanja vya ndege, tukianzia na Kiwanja cha Ndege cha Dar es Salaa, Mwanza, Tabora na Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizo, ningependa maeneo machache nayo nipate ufafanuzi. Nimuombe Waziri wa Uvuvi na Mifugo baadae naye aje atutolee ufafanuzi baadhi ya maeneo. Nimeangalia katika bajeti yake, nimeangalia katika hotuba ya Waziri wa Fedha, kwa kweli nimewapongeza sana eneo la mifugo au eneo la ufugaji, tozo nyingi sana zimeondoshwa, napongeza katika hilo. Lakini nilivyoangalia upande wa uvuvi, tozo zimebaki v ilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitaka kusafirisha kaa nje ya nchi leseni ni dola 2,500 na zamani ilikuwa unatoa leseni moja tu 2,500 umemaliza sasa hivi kila zao unalipa dola 2,500, ukitaka kaa dola 2,500, prawns dola 2,500, lobster dola 2,500 kwa hiyo kama unasafirisha mazao manne ujiandae dola 10,000. Lakini kila kilo ya zao unaposafirisha unalipa dola moja. Kwa kweli tutafanya wafanyabiashara katika eneo hilo washindwe kusafirisha mazao ya bahari na tushindwe kuvuna mazao ya bahari. Kwa hiyo, nitaomba Mheshimiwa Waziri wa eneo hilo uje ututolee ufafanuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilitaka kupendekeza kwenye Serikali, niipongeze kwa kuongeza tozo kwenye mafuta ghafi kufikia asilimia 25 kwa yale ambayo bado hayajachakatwa kabisa na asilimia 35 ambayo yamechakatwa mpaka hatua ya mwisho. Mheshimiwa Waziri, mimi naona bado hiki kiwango ni kidogo, hakitoshi. Kama kweli tunataka kuendeleza viwanda vyetu vya ndani, tuwe tunaangalia na soko la dunia linaendaje. Soko la mafuta ya chakula kila mwaka limekuwa likishuka zaidi. Kwa hiyo, mazao ya mafuta ya nje ni rahisi sana ukilinganisha na gharama za huku ndani. Pamoja na kuweka hizo asilimia, muwe mnaangalia na mwenendo wa mazao haya ya mafuta katika soko la dunia ili muwe mnafanya kama tunavyofanya diesel na petrol, bei zake ziwe zinabadilika na asilimia ya ku-charge iwe inabadilika kutegemeana na bei ya zao kule nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Waziri nipongeze kwa Serikali kuamua kuingia makubaliano na viwanda vya kuzalisha taulo za kikekwa sababu hiyo ndiyo itakuwa njia ya kuwanufaisha akina mama na sio kwa kupunguza zile kodi kwa sababu hakuna manufaa ya moja kwa moja kupitia msamaha wa kodi. Lakini kwa kuingia makubaliano, ina maana mtakubaliana mpaka bei hiyo ndiyo itawakomboa akina mama pamoja na watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili niungane na Wabunge wenzangu kuchangia katika bajeti hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Napenda kwanza kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Rais, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi kubwa sana aliyoifanya katika kipindi cha miaka mitano. Sina wasiwasi kabisa miaka mitano mingine ijayo tutaona mapinduzi makubwa sana ya kimaendeleo katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nianze kuchangia katika sekta ya afya na kabla sijaanza kuchangia sekta ya afya nimpongeze Makamu wa Rais, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu na nimpongeze Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Manaibu wake Mheshimiwa Kandege na Mheshimiwa Mwita pamoja na Katibu Mkuu na Manaibu wake kwa kazi kubwa sana wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwa upande wa sekta ya afya ndani ya kipindi cha miaka mine, tayari Serikali ya Chama cha Mapinduzi ya Awamu ya Tano imeanza kujenga na kukarabati hospitali za halmashauri 98, kati ya hizo 77 zimekamilika. Zitakapokamilika zote mwezi Juni, 2020 tutakuwa na hospitali za Halmashauri za Wilaya 175, ndio kusema tutabakiwa na Halmashauri tisa tu kujenga hospitali za wilaya ambazo nina uhakika kwa speed ambayo tunayo ndani ya mwaka mmoja wa mwaka 2020/2021 tutakuwa tumemaliza kabisa zoezi la kujenga hospitali za wilaya na hivyo kuifanya Serikali ya Chama cha Mapinduzi kuhamia kwenye ujenzi wa vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mtu ambaye anasema tangu tumepata Uhuru mpaka sasa hivi tumejenga vituo vya afya 900. Tanzania tuna kata 3,956 mpaka sasa hivi tumeshajenga vituo vya afya zaidi ya 900, ndiyo kusema kwamba tunahitaji chini ya miaka 10 kukamilisha ujenzi huu. Kwa sababu kama tumeweza kujenga vituo vya afya 433 ndani ya kipindi cha miaka 5, tunahitaji chini ya miaka 10 kukamilisha vituo vya afya 3,956. Kwa hiyo, yule aliyekuwa anasema tutahitaji zaidi ya miaka 20, hebu arudi kwa mwalimu wake wa hesabu na akazipitie tena zile hesabu.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

T A A R I F A

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hawa Ghasia, kuna taarifa, Mheshimiwa Mwakagenda.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji anayezungumza sasa, nimkumbushe tu kwamba tunamshukuru Jafo angalau kajitahidi, yeye alikuwa Waziri wa Wizara hii na alikuwa ni mwanachama wa Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, labda kama anatuambia anaomba msamaha kwa kwenda taratibu, hakufikia malengo. Nakupongeza Mheshimiwa Jafo kwa kufanya kazi nzuri. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tunapotaka kutoa taarifa tutumie zile Kanuni zetu vizuri. Hii siyo taarifa, Mheshimiwa Hawa Ghasia, endelea na mchango wako.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, anajifurahisha kwa sababu nimesema tumeongeza kutoka vituo vya afya 535 kwenda 968. Ndiyo kusema kuna kazi iliyofanyika siku za nyuma na tunaendeleza. Ndiyo maana nikasema tukikamilisha Hospitali za Halmashauri 98 tutakuwa na Hospitali za Halmashauri 175. Maana yake kuna kazi imefanyika siku za nyuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokisema speed imeongezeka na ndiyo maana nikasema kwa speed ambayo Mheshimiwa Jafo anayo, kwa speed ambayo Mheshimiwa Magufuli anayo…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. HAWA A. GHASIA: … tunahitaji chini ya miaka 10 kukamilisha ujenzi wa vituo vya afya katika nchi yetu. (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Esther Matiko, ungempa muda azungumze maana umeingia sasa hivi, umeshamsikia na mchango na taarifa unayo?

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa. Hadi nimesimama maana yake nimemsikia kuna kitu nataka nimpe taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hawa Ghasia, endelea na mchango wako. (Makofi)

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, wataelewa tu, naona wanaelewa kidogo kidogo na wanachangamka.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiacha hospitali za wilaya, Serikali ya Awamu ya Tano iko katika mchakato mpaka kufikia Juni, 2020 itakuwa kwa zaidi ya asilimia 60 imekamilisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini. Hata anayezungumza anafahamu kwamba katika Mkoa wake wa Mara kuna Hospitali ya Rufaa inajengwa na Chato pia inajengwa na zikikamilika hizo ndiyo kusema kwa maana ya Kanda tutakuwa tumekamilisha ujenzi wa Hopsitali za Rufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kutokea kule juu kwenye rufaa tunakuja kwenye hospitali za halmashauri, hospitali za mikoa, katika sekta ya afya, Mheshimiwa Magufuli akiingia awamu ya pili ana-deal na vituo vya afya na zahanati tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wale ambao wanasema kwamba hakuna kilichofanyika, hebu warudi waangalie tulikotoka, tulipo na tunakokwenda. Watakubaliana na mimi kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi inatekeleza Ilani yake kwa speed kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie tena kumpongeza Mheshimiwa Jafo kwa kusimamia vizuri elimu bila ada. Kama ambavyo tumesema, hili ni wazo la Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli la kuhakikisha kwamba watoto wote wa maskini wanakwenda shule na kuondoa ada katika shule zetu. Jambo hili limeongeza watoto wanaoandikishwa darasa la kwanza na hata wanaokwenda sekondari na imesaidia sana wazazi kujikita katika kuwapatia wanafunzi mahitaji mengine ambayo zamani ilikuwa wachangie ada na pia watafute na sare na vitu vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeongeza ujenzi wa vyumba za madarasa na ujenzi wa mabweni. Mimi ninayezungumza katika halmashauri yangu tunayo mabweni mawili ambayo yanaendelea kujengwa, tumepata pesa za kukamilisha maboma katika halmashauri yangu na miundombinu katika elimu ya sekondari na msingi imeboreshwa kwa kiasi kikubwa. Nichukue fursa hii pia kumpongeza sana Mkuu wangu wa Mkoa Mheshimiwa Blasius Byakanwa kwa ubunifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Serikali Kuu ilipojikita katika kukamilisha vyumba vya madarasa, kujenga nyumba za walimu yeye akaja na wazo la shule ni choo na akahamasisha wananchi, viongozi mbalimbali katika mkoa wetu na sasa hivi tunafanya vizuri sana katika kuhakikisha kwamba tunasaidiana na Serikali Kuu. Si kila kitu kuiachia Serikali, tunakuja tunasimama hapa tunasema kitu fulani hakijakamilika, sisi kama sisi na wananchi wetu tumefanya nini?

Kwa hiyo, nimpongeze sana Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa kwa kuja na wazo la shule ni choo pamoja na mengine yale ambayo yako katika mchakato mzuri sana, nina imani kabisa tutamsaidia katika kupitisha sheria ili gongo sasa ikawe sanitizer. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuanzisha Mamlaka ya Wakala wa Barabara Vijijini (TARURA). TARURA imefanya kazi nyingi sana na kubwa sana. Nachoiomba Serikali ni kuiongezea vyanzo vya mapato. Pesa wanayopewa TARURA na kazi waliyonayo ni tofauti. Tunaomba tuwaongezee na tuwatafutie vyanzo vya uhakika vya mapato ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naunga mkono hoja. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Jafo pamoja na Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2017.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami napenda niungane na wenzangu kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Muswada wa Sheria ya Fedha kwa Mwaka 2017. Kwa kweli sikuhitajika nisimame nichangie kwa sababu Wizara ya Fedha imechukua karibu zaidi ya asilimia 80 mapendekezo ya Wabunge na ya Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, isipokuwa nimesimama kuweka sawa baadhi ya mambo ambayo yanaonekana yanapotoshwa kwa makusudi kwa misingi ya kujitafutia umaarufu wa kisiasa wa kirahisi rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kwanza ambalo nataka nilisemee ni kuhusu kupata Miswada miwili. Wakati nawasilisha hotuba yangu nilisema kwamba Miswada hii huu wa pili ni matokeo ya mchakato mzima wa majadiliano yaliyoanzia kwenye Kamati za Kisekta, Kamati ya Bajeti na kupitia katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria zilizoongezwa kwanza ni Sheria ya Posta na Mawasiliano ya Kieletroniki. Sheria hii imependekezwa kupitia katika Kamati yangu, tukiomba suala la uuzaji wa share lisiishie kwa Watanzania peke yake, liende mpaka kwa watu wengine ili kuhakikisha kwamba tunavuta mitaji lakini tunachangamsha soko letu la mitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili wakati tunatoa hayo mapendekezo Mheshimiwa Msemaji wa Kambi ya Upinzani alikuwepo na yeye ni miongoni mwa waliochangia, sasa sijui kwamba wakati tulivyokuwa tunaiomba Serikali tulitaka watuambie kwamba walichukue mpaka mwakani? Nilitegemea kwamba tupongeze kwa Serikali kuchukua yale ambayo tumeyapendekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Sheria ya Michezo ya Kubahatisha, tumependekeza ndani ya Bunge. Sheria ya Usalama Kazini tumelalamika kwamba kumekuwa na suala la ukaguzi wa mara kwa mara ni kero, ni usumbufu. Kama Waziri amekuja na Muswada ambao vitu hivyo havimo, Wabunge tumeomba, Serikali imekubali, imeongeza hizo sheria, badala ya kushukuru Serikali tunasema tumeshtukizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwahakikishia…

T A A R I F A ...

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, siipokei kwa sababu wakati tunajadili haya mambo mpaka tunaafikiana alikuwa ni mtoro, akiingia, anatoka. Kwa hiyo, hawezi akajua tulifikiaje katika marekebisho hayo. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme kwamba haya yaliyoletwa na Serikali kama ziada ni mapendekezo ya Kamati, ni mapendekezo ya Wajumbe, nami naipongeza sana Serikali, nampongeza sana Waziri wa Fedha na Mipango kwa kupokea mapendekezo ya Kamati na kuyafanyia kazi na kuandika upya Muswada wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Mwanasheria Mkuu wa Serikali isipokuwa wale wenzetu walipenda, kwamba yale tuliyomshauri Waziri wa Fedha asiyakubali ili waje walalamike kwamba Waziri huyu siyo msikivu. Sasa anakuwa msikivu wanalalamika, sijui tuwekwe wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo napenda nilichangie, sikuwa na sababu ya kuchangia kwa sababu bajeti ni nzuri. Suala la kusema kwamba tumeanza sera za ubaguzi ndani ya Bunge hili. Hakuna ubaguzi, tulichokiuliza na ambacho tunasimamia ni suala la kukaa zaidi ya miezi mitatu hapa tunaijadili bajeti, tunatoa mapendekezo, Serikali inayachukua, halafu mtu anakuja anasema siungi mkono, au anasema hapana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na njia tatu, ulikuwa na uwezo wa kusema hapana, ulikuwa na uwezo wa kusema ndiyo na ulikuwa na kusema sina maamuzi. Huna maamuzi kwa sababu yapo uliyoyakubali na yapo ambayo hujayakubali. Hakuna aliyesema kwamba hana maamuzi, badala yake wamesema wanakataa, sasa kama bajeti umeikataa…

T A A R I F A ...

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, siipokei kwa sababu napongeza pale napopongeza, nisipokubaliana na hilo ninatoa ushauri jinsi gani Serikali yangu ifanye na pale Serikali yangu inavyochukua ule ushauri wangu nilioutoa ndipo ninapokuja nasema naunga mkono Bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wazima hivi au ile maana ya abstain watu hawakujua maana yake ndiyo maana hakuna hata mtu mmoja aliyesema abstain. Waswahili wanasema ukiligoroga lazima ulinywe, mmeikataa bajeti kwa hiyo madhara ya kukataa bajeti lazima yawafikie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru naona sindano zangu zimeingia vizuri sana na ndiyo maana watu wote sasa wanashindwa, wanagugumia kama ambavyo watoto wakichomwa sindano wanalia. Poleni sana mwakani mjifunze jinsi ya kuunga mkono bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.