Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Suleiman Ahmed Saddiq (13 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi asubuhi ya leo na mimi niwe miongoni mwa wachangiaji katika hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa hapa Bungeni tarehe 20 Novemba, 2015 hapa Bungeni. Awali ya yote, naomba
kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayofanya; na niwaombe sana Watanzania wote tumwombee na tumtakie heri aweze kutimiza malengo yake kwa faida ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana wananchi wa Mvomero kwa kunikumbuka tena kwenye ufalme wao, hatimaye nimerudi tena mjengoni. Nawashukuru sana na ninawaahidi sitawaangusha. Nawaahidi wananchi wa Mvomero sitawaangusha, ujinga ni pa kwenda siyo pa kurudi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana nichangie hotuba ya Mheshimiwa Rais katika maeneo mbalimbali na pia nimpongeze kwa juhudi kubwa aliyoianza katika kuboresha uchumi wa Taifa, katika kupambana na mafisadi, katika kuboresha mapato ya nchi yetu. Bado tuna
mianya mingi, bado tuna kazi kubwa ya kumshauri na kumsaidia Mheshimiwa Rais wetu. Yapo majipu mengine yeye hayajui, sisi tunaoishi na wananchi, tunaokaa kwenye Halmashauri tunayafahamu, ni wajibu wetu tumsaidie ili sasa turudi kwenye mstari. Taifa hili lina kila aina ya
neema, ni nchi ambayo ina baraka kubwa za Mwenyezi Mungu. Tuna maziwa, tuna madini, tuna bahari, tuna ardhi kubwa, ni nchi ambayo inatakiwa isonge mbele kimaendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na suala la wakulima na wafugaji. Katika Taifa letu lipo tatizo kubwa la wakulima na wafugaji hasa katika Wilaya yangu ya Mvomero. Eneo hili linahitaji kazi ya ziada. Nami napenda kuishauri Serikali kupitia kwa Wizara ya Ardhi, Wizara ya
TAMISEMI, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Mifugo na Kilimo na Wizara ya Maliasili zishirikiane kwa pamoja. Hawa wote ni wadau wakubwa katika eneo hili la kuondoa tatizo la wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna tatizo kubwa kwenye maeneo yetu lakini bado tuna maeneo ambayo ni hifadhi. Hifadhi zile zinabaki kuwa hifadhi, lakini baadhi ya maeneo ya wakulima wanahangaika, wafugaji wanahangaika, hifadhi nyingine hazina tija kwa Taifa letu. Namwomba sana Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kama Waziri wa Kilimo, aliangalie hili, ashirikiane na wadau wenzake, tuwapatie maeneo wafugaji, tuwapatie maeneo ya ziada wakulima na tuweke sheria thabiti kuondoa maafa, kuondoa machafuko kati ya wakulima na wafugaji. Tukiweka utaratibu huo mzuri, nasi kwenye Halmashauri zetu tukatengeneza sheria za kuwadhibiti tutaleta maendeleo ndani ya kilimo, ndani ya ufugaji. Kwa kuwa muda ni mdogo, naomba niende haraka haraka.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niingie kwenye suala la uchumi. Naiomba sana Serikali ifanye kazi ya ziada kwa kuhakikisha kwamba tunaweka sera nzuri za kuendelea kuwatambua wafanyabiashara, kwa maana ya sekta binafsi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna nchi yoyote duniani ambayo imesonga mbele kiuchumi bila sekta binafsi. Sekta binafsi ni mhimili mkuu wa Taifa. Sekta binafsi inaweza ikaongeza pato la nchi yetu, lakini katika sekta binafsi wapo wafanyabiashara wana upungufu.
Ni vyema sasa tukaweka utaratibu mzuri, tushirikiane na sekta hii kukuza viwanda na uchumi wetu. Yapo mambo mengi kwenye sekta binafsi yanatakiwa yashughulikiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kwamba Mheshimiwa Rais ana ndoto kubwa ya viwanda katika Taifa letu. Tatizo lililopo katika suala zima la viwanda ni sera za nchi yetu. Yapo maeneo sera zinatubana. Ni vyema tukakaa tukarekebisha sera zetu, tukaangalia
wapi tulikosea, wapi tupo na mabadiliko ya dunia ya leo yanasemaje. Tukibadilika katika utaratibu huo, sasa tunarudi kwenye kuanzisha na kusimamia viwanda. Hapo tutasonga mbele kwa hatua kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala la baadhi ya wafanyabiashara kutokuwa waaminifu. Naomba wanaohusika na masuala ya bajeti, wanaohusika na masuala ya uchumi, mfanyabiashara mwenye kiwanda cha mafuta ana-declare analeta crude oil kumbe anadanganya analeta semi. Hawa ndio ambao wanadunisha, viwanda haviendelei, tunarudi nyuma, wao wananufaika. Wanacheza na Kamati ya Bajeti, wanacheza na wahusika, wanaingiza mambo yao kwenye bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha nina imani na wewe, najua uzoefu wako, anza kupambana na mambo haya katika bajeti ya mwaka huu. Usiruhusu wenye viwanda vya ndani walete udanganyifu. Tunachotaka, uchumi ukue tupate maendeleo.
Mvomero tunahitaji barabara ya lami ikamilike, Mvomero tunahitaji umeme ufike vijiji vyote, Mvomero tunahitaji leo maji yafike maeneo yote. Lakini maji yale hayatafika kama uchumi utalegalega. Tutaisaidia Serikali, tutakaa na Mawaziri, dakika kumi hazitoshi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la umeme. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri mhusika, lakini ushauri wangu katika suala la umeme tuongeze nguvu zetu katika kuzalisha umeme wa maji na umeme wa gesi badala ya kutegemea umeme wa mafuta
ambao unawanufaisha wafanyabiashara na Taifa tunabaki nyuma.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono juhudi zote, umeme wa maji, umeme wa gesi na umeme wa mafuta haufai, haufai, haufai! Umeme wa mafuta ni biashara ya wakubwa. Wamejiandaa, wana mambo yao, wanafanya kazi zao. Sisi tuongeze nguvu kwenye gesi, maji
na kwenye umeme wa upepo. Najua bado dakika zinaniruhusu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la vocha za mbolea. Kuna tatizo kubwa sana vijijini, kuna watendaji ndani ya Serikali ndani ya Halmashauri zetu sio waaminifu. Baadhi yao vocha hizi wananufaika wao badala ya kumnufaisha mkulima wa kijijini.
Mheshimiwa Mwigulu nakuaminia sana, umefanya kazi nzuri na unaendelea kufanya. Tuendelee kukusaidia kama Wabunge ili uboreshe eneo hili kwa faida ya nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la uchaguzi wa Zanzibar ni suala la kisheria. Tuwatakie Wazanzibar uchaguzi mwema. Wanaopiga kelele, waendelee kupiga kelele, uchaguzi umetangazwa unarudiwa. Mheshimiwa Rais hawezi kuingilia tena. Tume ya Uchaguzi Zanzibar
imetangaza uchaguzi urudiwe, tuwatakie uchaguzi mwema tarehe 20 Machi. Tutampata ambaye atachaguliwa kwa haki. Mizengwe mizengwe iliyokuwepo nyuma ndiyo imesababisha uchaguzi ule umefutwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuwe wa kweli. Sasa hivi tumtakie mema Rais wetu afanye mambo mengine makubwa, tusimchanganye. Tumepata Rais ambaye anaweza kutuvusha hapa tulipo, haogopi, ni mkweli, ni mwaminifu kwa Taifa lake. Ana ndoto nyingi ambazo
anahitaji kuzitimiza kwa Taifa lake. Tumpe ushirikiano, tuache maneno maneno, tusonge mbele. Kama mlikuwa mna uchungu, mngemsikiliza Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja mia kwa mia. Nawatakia kila la heri Watanzania wote. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA VIWANDA, BIASHARA NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru tena kwa kunipa nafasi kwa mara nyingine niweze kuhitimisha hoja ya Kamati ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naomba niwashukuru sana wachangiaji wote waliochangia hoja hii, wale ambao wamechangia kwa maandishi na wale ambao wamechangia kwa kuzungumza Bungeni. Waliochangia kwa kuzungumza Bungeni ni wanane na naomba kwa haraka haraka niwatambue, Mheshimiwa Lulida, Mheshimiwa Kamala, Mheshimiwa Jitu, Mheshimiwa Kuchauka, Mheshimiwa Janet Mbene, Mheshimiwa Silinde, Mheshimiwa Hussein Bashe na Mheshimiwa Livingstone Lusinde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale ambao wamechangia kwa maandishi ni 11, naomba nao niwatambue; Mheshimiwa Pascal Haonga, Mheshimiwa Zainabu Amiri, Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mheshimiwa Nuru Bafadhili, Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mheshimiwa Oran Njeza, Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mheshimiwa Lucy Owenya, Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mheshimiwa Suzana Chogisasi na Mheshimiwa Juma Othman Hija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeamua niwatambue hawa kwa sababu wengi wamezungumza hoja ambazo zinafananafanana, wale ambao wameleta kwa maandishi na wale ambao wamezungumza hapa Bungeni. Pia naomba niwashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri kwa ufafanuzi wa hoja mbalimbali. Naomba niwashukuru sana Mheshimiwa Waziri January Makamba, Mheshimiwa Mwijage na Mheshimiwa Dkt. Mpango, nawashukuru sana kwa ufafanuzi wa hoja mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingi ambazo zimezungumzwa ziko katika maeneo tofauti tofauti. Kuna hoja ambayo imezungumzwa sana na Wabunge wengi ni kuhusu Mamlaka nyingi za Udhibiti. Wabunge wametoa michango yao, wametoa ushauri wao lakini na sisi kama Kamati tulishayaeleza haya na ni matumaini yetu kwamba Serikali itayafanyia kazi haya masuala ili kupunguza utitiri huu wa mamlaka na kuleta utaratibu mzuri wa uzalishaji katika viwanda na biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezitaja zile mamlaka zote ambazo zinaingiliana katika usimamizi wa viwanda, mfano OSHA, NEMC, TFDA, TBS na wengine wengi. Kwa hiyo, ni hoja ambazo zimekuja lakini na sisi kama Kamati tulishapendekeza nini kifanyike, ni matumaini yetu Serikali itakuwa imepokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na suala lingine la ubinafsishaji wa viwanda. Katika hotuba yangu ukurasa wa 33 na 63 tumelizungumza kwa kina. Viwanda ambavyo taarifa tumeletewa kwenye Kamati viko 156 vimebinafsishwa na Serikali inaendelea kuvifanyia kazi vile viwanda lakini Wabunge wameeleza kwa masikitiko makubwa na wengine wamediriki kusema kwamba hatua kali zichukuliwe kwa wale ambao wamepewa viwanda vile lakini havizalishi, Serikali imekosa mapato kwa kipindi chote cha miaka ambayo viwanda vile vimebinafsishwa. Viwanda vingi vimebinafsishwa kati ya mwaka 1997, 1998, 1999 mpaka 2000, utaona ni miaka mingi sasa Serikali imepoteza mapato mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili wapo Wabunge wamesema kwamba hatua ambazo zitachukuliwa ni pamoja na kulipa kodi kwa miaka yote ambayo viwanda vile havikufanya kazi. Wapo Wabunge wameshauri kwamba lipo suala la viwanda hivi vilivyobinafsishwa, wawekezaji wale wamechukua hati wamezipeleka benki, wamekopa na matokeo yake hati zile zimekaa benki lakini viwanda vile havikupata fedha zile, fedha zimeingia kwenye biashara zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mambo ambayo Kamati ilishayapendekeza, ni matumaini yangu kwamba Serikali itayafanyia kazi. Mheshimiwa Waziri amejibu kwamba hili jambo lipo katika hatua za utekelezaji, Kamati inasisitiza utekelezaji ufanyike kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo suala la Mradi wa Kurasini (Kurasini Business Park), Kamati imezungumza muda mrefu na Mheshimiwa Waziri amelijibu. Ni matumaini yetu kwamba jambo hili sasa litashughulikiwa kwa uharaka mkubwa ili eneo lile sasa lianze kuzalisha Watanzania wapate ajira, Serikali ipate mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumzwa na Wabunge wengi ni suala la Kiwanda cha General Tyre. General Tyre ya Arusha Kamati tumeizungumza sana, tumetoa ushauri wetu, Serikali imesikia na leo hoja hii imejibiwa ni matumaini sasa msukumo mkubwa utaanza. Nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha, katika hili la General Tyre na yeye aweke mkono wake kwani Wizara ya Viwanda peke yake hawataweza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha suala la General Tyre liwe ni suala la umoja wote Wizara ya Fedha, Wizara ya Viwanda na Wizara nyingine tushirikiane. Zipo hatua ambazo zimechukuliwa na tunaomba Serikali iandae mazingira rafiki ya uwekezaji katika General Tyre. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa suala la bidhaa feki za pombe na sticker fake, hili limepokelewa na Kamati yetu na Serikali itakuwa imelisikia, imelipokea litafanyiwa kazi. Eneo hili linapoteza sana mapato. Bidhaa feki kwanza zinaharibu afya za Watanzania, lakini pia Serikali inakosa mapato. Hili limechukuliwa na litafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lipo suala la TBS na TFDA, Wabunge wamelizungumza sana. Naomba niseme kwa kifupi sana, TBS wao kazi yao ni bidhaa za viwandani, TFDA wao kazi yao ni bidhaa ambazo zinakwenda moja kwa moja kwenye madawa na vyakula. Kwa hiyo, pale kuna utaratibu tofauti kabisa, sasa wanapoingiliana wale hatujui ni kwa nini wanaingiliana. Kila mmoja ana eneo lake, kuna bidhaa za madawa na bidhaa za chakula na yule ana bidhaa za viwandani. Tunaomba Mamlaka hizi zipewe eneo la mipaka ya kazi ili kupunguza urasimu ambao wafanyabiashara wanaulalamikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilipongeze suala la umeme. Leo asubuhi tumezungumza kwamba Mkoa wa Tanga, Mkoa wa Morogoro walikuwa wana ration ya umeme, wanaambiwa viwanda vizalishe usiku na mchana wasizalishe. Kwa taarifa niliyoipata leo kupitia kwa Waziri kwamba lile zoezi lilikuwa ni la muda, ukarabati umeshafanyika, sasa hivi viwanda vinazalisha usiku na mchana. Hili nalipongeza sana Serikali na Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana kwa kutatua tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Wakala wa Vipimo, Wabunge wameshauri Wakala huyu ashuke chini ili mazao ambayo yanakwenda sokoni wale wakulima na wazalishaji wapate haki yao ya vipimo. Vipimo viende sambamba na uzalishaji. Tunaiomba Serikali ilifanyie kazi hili na Wakala huyu aongeze nguvu katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo suala limezungumzwa la utitiri wa kodi. Suala hili nimwombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Kamati yetu kupitia CTI ambayo walikuja wametuletea orodha ndefu ya utitiri wa kodi. Kodi nyingine zinarudiarudia, wafanyabiashara wanapata shida na wakati mwingine wanapata matatizo jinsi ya kulipa zile kodi. Tunaomba Serikali ilifikirie jambo hili na wafike mahali waanze kukaa na Kamati ya Bajeti, Kamati ya Viwanda na Kamati zingine ili walifanyie kazi kwa ndani zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la mifuko ya plastiki, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri January Makamba amelisemea vizuri na Kamati imependekeza lazima tufike mahali sasa mifuko ya plastiki iwe basi. Kamati katika eneo hili imependekeza Wizara itafute namna nyingine, tupate viwanda mbadala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bidhaa zingine zinazobebwa zinahitaji mifuko, kwa hiyo, Wizara iharakishe kutafuta viwanda mbadala au wenye viwanda hivyo ambavyo wapo wapewe teknolojia ambayo itawasaidia kuzalisha mifuko mbadala ikiwemo mifuko ya karatasi, nguo, majani na mifuko mingine ili tunapoondoa mifuko tuweke mifuko mbadala. Kamati imependekeza hilo, ni matumaini yetu Wizara imesikia na Wizara ya Viwanda nao watakuwa wamelisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo tunapenda sana kuliunga mkono ni suala la uchafuzi wa mazingira. Kuna viwanda kwa makusudi wanachafua mazingira kwa kutumia Tanzania ya Viwanda. Hii dhana hii wanaitumia vibaya. Tunaomba Wizara hii, Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira kazeni buti wale wanaochafua mazingira sheria ichukue mkondo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa mengi na sisi tunasema tumeyapokea kama Kamati lakini Kamati nayo asubuhi wakati tunawasilisha taarifa yetu tulitoa maoni na mapendekezo yetu. Naomba Waheshimiwa Wabunge mapendekezo yetu yale tutayachukua pamoja na ya kwenu mliyotuletea leo kwa maandishi pamoja na kwa kuzungumza tutayachanganya pamoja ili tuyapeleke katika taasisi zinazohusika yafanyiwe kazi kwa faida ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila ya kuchelewesha muda, naomba sasa nikushukuru wewe, niwashukuru Mawaziri wote waliochangia, lakini pia niwashukuru sana Wajumbe wa Kamati yangu kwa jinsi ambavyo tumekwenda pamoja katika suala hili. Maoni yetu ya mwisho na maazimio yetu, wawekezaji wawe wakweli kwa Taifa lao. Wawekezaji watoe taarifa sahihi Serikali iweze kuwasaidia na walipe kodi Serikali iweze kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Kamati tunawashauri wawekezaji wawe wakweli kwa Serikali, watoe taarifa sahihi na sisi kama Kamati tutawalinda na tutawasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ombi letu la pili tunaomba Watanzania wapende bidhaa za Tanzania. Unapopenda bidhaa za Tanzania, unaunga mkono juhudi za Serikali ya Tanzania ya Viwanda lakini tunamuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu. Kwa hiyo, tunaomba Watanzania wapende bidhaa za Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba Serikali iendelee kuboresha mazingira mazuri kwa wafanyabiashara, mazingira rafiki kwa wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa nihitimishe hoja yangu kwa kuwaahidi kwamba Kamati yetu imeyapokea masuala mbalimbali na yale ambayo tumeyatoa asubuhi pamoja na haya ya jioni ya leo tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa kutoa hoja, mapendekezo yote ya Kamati yapokelewe na yafanyiwe kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli. Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa sana, kazi anazofanya matunda yake tunayaona. Leo nimefarijika sana kusimama mbele ya Bunge hili na kutoa shukrani za dhati kabisa kwake kwa kazi kubwa anayofanya hatimaye leo tuna bajeti nzuri sana ya Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, wamejipanga vizuri, wanafanya kazi nzuri na ni wasikivu. Niliwaomba Bunge lililopita tuna tatizo Mvumero, mvua zimenyesha na daraja limekatika, moja kwa moja hawakuwa na kigugumizi waliniambia twende na siku ya Jumamosi niliondoka nao tulienda Mvomero. Waziri alitoa maelekezo ndani ya siku saba daraja lile kingo zote zilitengenezwa. Hii ndiyo kasi ya Magufuli, nawapongeza sana kwa kazi kubwa wanayofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ambalo napenda kuchangia ni Kurasini, upande wa bandari yetu. Eneo la Kurasini kuna msongamano mkubwa sana wa malori. Malori yale sasa hivi yanasababisha msongamano ule unaendelea hadi Kibaha. Niwaombe wenzetu watafute namna bora na kutafuta eneo lolote kujenga haraka dry port kati ya Kibaha na Morogoro ili tuondoe msongamano ule, tuboreshe miundombinu na uchumi usonge mbele. Bandari na barabara zinapanuliwa lakini bado malori yale yanaleta msongamano kubwa sana. Malori ya mafuta na makontena hali imekuwa mbaya. Tunaomba wenzetu walifanyie kazi, nina imani wanalifahamu hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba pia nizungumzie kidogo tu daraja la Kigamboni. Kazi iliyofanywa ni kubwa sana, daraja zuri na la mfano. Nimuombe Waziri katika maeneo mawili, tunajua gharama iliyotumika pale ni kubwa, magari ya abiria hususani daladala wanaovuka kwenye daraja lile wanalipa shilingi 7,000, daladala ambayo imepakia watu 30, akimtoza abiria shilingi 400; anapata shilingi 12,000 akilipa shilingi 7,000 kabaki na shilingi 5,000. Serikali hii ni sikivu jaribuni kulifanyia kazi jambo hili, kwa magari ya abiria tariff ipunguzwe. Tunaweza tukaweka shilingi 2,000 au shilingi 1,500/=, magari mengine yote Lexus, VX, hata shilingi 10,000/= watu watalipa, lakini magari ya abiria tuyaangalie. Tupunguze kidogo ili wananchi wetu waweze kufaidika na matunda ya daraja lile.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia suala la baiskeli, kuna mtu ana madafu na machungwa yake anatoka Kigamboni anafika pale anatozwa hela nyingi. Naomba baiskeli nazo zisaidiwe wengine wote waendelee kulipa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri haya mawili naomba uyafanyie kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie suala la uwanja wa ndege wa Dar es Salaam (Terminal II). Pale kuna msongamano mkubwa, wakati tunaendelea kusubiri Terminal III upande wa arrival, kuanzia saa saba mchana mpaka saa tisa au saa kumi, ndege ni nyingi, mizigo ina-delay sana kutoka kwenye ndege kuja eneo la abiria. Tunaomba juhudi za haraka zifanyike ili abiria wasikae muda mrefu. Ndege zinagongana, moja inaingia saa saba, nyingine saa nane na nyingine saa sita, naomba sana suala hili lifanyiwe kazi, wakati tunaendelea kusubiri matunda mazuri ya Terminal III. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba niingie Mvomero. Mvomero tuna daraja ambalo nimemshukuru Mheshimiwa Waziri kazi nzuri imefanyika. Sasa hivi tuna mradi wa barabara ya lami kutoka Magole – Turiani - Handeni. Mpango wa barabara hii tokea mwanzo ilikuwa lami iwekwe Korogwe - Handeni, Handeni-Turiani, Turiani-Magole ili Magole pale magari yote yaelekee Dodoma na Kanda ya Ziwa, abiria wa Mombasa, Tanga na maeneo mengine wapite barabara ile ya shortcut. Naishukuru sana Serikali mwaka huu Mheshimiwa Waziri ametenga fedha nyingi kumalizia kilometa 48 za awali kutoka Magole – Turiani, hilo tunalishukuru sana na wananchi wanasubiri kazi ianze.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika hili mkandarasi anadai fedha za nyuma, naomba Mheshimiwa Waziri ili aanze kazi mngekaa naye mkamaliza madeni ya nyuma. Kampuni ya Kichina inadai fedha kidogo za nyuma, hapa mme mtengea fedha nyingi, malizaneni naye aanze kazi mara moja. Naomba barabara ya kutoka Turiani - Mzia - Handeni ambayo tayari mmeshafanya upembuzi yakinifu, tengeni fedha tufungue mlango wa lami Korogwe mpaka Magole kuelekea Dodoma na Kanda ya Ziwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimkumbushe Mheshimiwa Waziri, kuna ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, barabara ya kutoka Chuo Kikuu Mzumbe, wanaita Sangasanga – Langali - Mgeta. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne alituahidi barabara ile itajengwa kwa kiwango cha lami. Naona mwaka huu wametenga fedha shilingi milioni 700 kwa kilometa mbili, sijui lami nyepesi au nzito sielewi. Naomba suala hili Mheshimiwa Waziri nikukumbushe kwa niaba ya wananchi wa Mvomero ili ahadi ile ikamilike tuendelee kupata matunda mazuri ya Serikali ya CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la minara ya simu nimeshakwenda kwa Mheshimiwa Waziri mara nyingi na aliniambia kuna mpango wa kupeleka mnara Kibati. Kwenye kitabu chake cha mawasiliano, ukurasa wa 18, namba 272 na 273 ameonesha kuna mnara Kanga na Kibati na minara hii imetengewa fedha nyingi, mnara mmoja anasema haujawaka, mwingine umewaka. Mheshimiwa Waziri minara yote haipo, hakuna uliowaka na hakuna ambao umezimwa. Mheshimiwa Waziri nilimpa kilio changu cha wananchi wa Kibati na akaniunganisha na watu wa Halotel…
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja mia kwa mia.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA VIWANDA, BIASHARA NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nikushukuru sana wewe kwa kunipa nafasi tena kuja kumalizia shughuli ambayo tumeianza asubuhi ya leo. Pia naomba nikushukuru kwa mara ya pili kwa jinsi ulivyoweka mstari katika suala lililozungumzwa na Waziri wa Fedha. Waziri wa Fedha ameleta habari njema, amezungumzia kwamba ile refund ya industrial sugar ya 15% Serikali imeanza kulipa na wameanza kulipa tokea Desemba na wewe ukaweka mkazo hivi hakuna watu wenu wakalieleza hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Kamati tulilizungumza hili muda mrefu, tulipata vilio vya wenye viwanda, wakasema mitaji yao imeganda, imekwama, wanashindwa kuendelea na uzalishaji na wengine wakatishia hata kufunga viwanda. Leo Serikali imefanya kazi kubwa, wameanza kulipa; Kamati ilikuwa ipaswe kuambiwa mapema. Mheshimiwa Dkt. Mpango tunakushuru sana kwa hili na niishukuru sana Wizara kwa kuanza kulipa na tuwaombe kama Kamati waendelee kulipa, bado kuna wengine wamebaki endeleeni kuyafanyia kazi. Hii ni Serikali sikivu na sasa ni kweli Tanzania ya viwanda imeanza kusikilizwa, hongera sana kwa Mheshimiwa Dkt. Mpango na hongereni sana Wizara zote zinazosimamia jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuwashukuru wachangiaji wote waliochangia katika hotuba ya Kamati ya Viwanda na Biashara, niwashukuru Wabunge wote lakini naomba kwa sababu ni wachache mno niwatambue. Waliochangia kwa kuzungumza ni Waheshimiwa Wabunge 15; Mheshimiwa Mwambe, Mheshimiwa Kishimba, Mheshimiwa Kiteto, Mheshimiwa Musukuma, Mheshimiwa Mndolwa, Mheshimiwa Lema, Mheshimiwa Millya, Mheshimiwa Nsanzugwanko, Mheshimiwa Amon, Mheshimiwa Komu, Mheshimiwa Mbatia, Mheshimiwa Mwigulu, Mheshimiwa Genzabuke na Mheshimiwa Mollel pamoja na Makamu Mwenyekiti Kanali Masoud. Nawashukuru sana wote hao waliochangia kwa kuzungumza na kuna mmoja amechangia kwa maandishi Mheshimiwa Peter Lijualikali. Nawashukuruni sana wote ambao mmeunga mkono na kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ambao yamezungumzwa sana katika michango ya Wabunge ni maeneo ambayo tumeyasema sisi kama Kamati, maeneo ambayo Kamati imeiomba Serikali iyafanyie kazi haraka, maeneo ambayo Kamati ilishaomba Serikali au ilishawashauri Serikali kuyashughulikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza lilikuwa ni suala la VAT refund ya 15%; wapo Wabunge wamelizungumza sana hili na Serikali imeanza kulishughulikia. Naipongeza sana Serikali katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni viwanda vilivyobinafsishwa; hapa katika eneo la viwanda vilivyobinafsishwa kuna shida kidogo. Kuna shida kwa sababu zile data ambazo tumeletewa sisi kama Kamati na hizi data ambazo zinaendelea kutolewa haziendi sawa. Sisi Kamati na Wizara tunatakiwa wote tunyooshe mstari. Waziri anaposema viwanda vinavyofanya kazi vizuri sana 68 sisi tunasema sio 68, kwa hivyo hatuendi vizuri. Nitaomba Mheshimiwa Waziri tukae tuyaweke sawa haya mambo na Kamati ilikuwa inaomba sana tupate data za uhakika kwa sababu nia na madhumuni wote twende kwenye mstari ulionyooka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili la viwanda vilivyobinafsishwa limebeba eneo kubwa la uchumi wa nchi yetu. Viwanda hivi vingine vinakosesha ajira, Serikali inakosa mapato, lakini kubwa zaidi Watanzania wanakosa bidhaa. Viwanda hivi vingine vilikuwa vina mitaji, wengine walikuwa wana business plan nzuri, wengine wamekopa mabenki, leo viwanda vingine havipo na mashine hazipo. Kwa hiyo, tunaomba eneo hili Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia Serikali muwe sikivu sana katika eneo hili. Tunaomba maazimio yetu yafanyiwe kazi kwa ubora wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumzwa sana ni suala la Liganga na Mchuchuma. Kamati ilishauri kwamba suala hili linahitaji uwekezaji mkubwa na Kamati imeshauri kwamba kama inawezekana tungeanza kuuza raw material, ile raw material tukianza kuuza gharama zitakuwa ni ndogo lakini tukisema tujenge kiwanda gharama bado ni kubwa, kutahitajika gharama za kila aina. Kwa hiyo, ni matumaini yetu kwamba suala hili Serikali imeliona na nashukuru kwa majibu mazuri ambayo Mawaziri wameanza kuyatoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo Wabunge wamelizungumza zaidi ni mazingira ya kufanyia biashara. Ni kweli kulikuwa na tatizo ambalo ni kubwa, Serikali imekuwa sikivu, Mheshimiwa Rais ameshafanya vikao mbalimbali na private sector, Wizara wameshafanya mikutano mbalimbali na wadau na sisi kama Kamati tumeshashiriki kwenye baadhi ya mikutano yao. Ombi letu kama Kamati ile mikutano ya wadau iendelee, iwe ni mikutano ya mara kwa mara. Tutakuwa tunapata changamoto na kuzitatua haraka iwezekanavyo. Vikao kama vile inaonekana vimesitishwa, tunaiomba sasa Serikali ianze kuvifufua vikao vile na mazungumzo ya mara kwa mara yaendelee kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kuipongeza Serikali, zipo tozo ambazo zimeanza kuondolewa. Zipo tozo ambazo zilikuwepo kwenye blue print wameanza kuzianyia kazi kwa upande wa OSHA zipo tozo tano zimeondolewa. Kwa hiyo, Kamati yale ambayo imependekeza yameanza kushughulikiwa lakini bado tunahitaji iende kwa kasi zaidi kwa sababu malalamiko ni mengi kuliko vile yanavyoshughulikiwa. Inaonekana kuna mwanga kwamba kazi imeanza kufanyika na naipongeza sana Serikali. Naipongeza sana Serikali kwa sababu sasa hivi Mheshimiwa Rais ametuwekea Wizara ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hii Wizara ya Uwekezaji tuna matumaini makubwa kama Kamati kwamba, tutafanya kazi kubwa, tutapata wawekezaji wengi na wawekezaji wengi watakuja kwa sababu Serikali ni sikivu. Katika hili nimpongeze Mheshimiwa Waziri Angella leo amezungumza maneno ya maana sana na ameunga mkono juhudi zote za Kamati, kwa pamoja tutafika Mheshimiwa Waziri karibu sana kwenye Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mengine limezungumzwa suala la wafanyabiashara kukaa pamoja, hili lilianza kufanyika; Serikali ilianza kukaa pamoja na wafanyabiashara. Tunaomba utaratibu ule uendelee na Mheshimiwa Rais tunampongeza na yeye mwenyewe kwa juhudi zake, alishakaa na taasisi mbalimbali, alishazungumza suala la kodi na tozo na matumaini yangu kwamba mambo haya sasa yanaanza kushughulikiwa hatua kwa hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Kiwanda cha Urafiki, kiwanda hiki kinasuasua muda mrefu na kiwanda hiki kimepata mwekezaji ambaye toka ameingia ni hasara, hakuna faida yoyote kwenye Kiwanda cha Urafiki. Ajira zilikuwa 2,000, sasa hivi kuna ajira chini ya 400; kiwanda kilikuwa kinapata faida, sasa hivi ni hasara kwa miaka na miaka. Kamati inaomba juhudi za haraka zichukuliwe, Urafiki ilikuwa inazalisha mazao mazuri, vitenge vizuri, Watanzania wengi walikuwa wanakimbilia pale. Tunaomba juhudi za haraka zichukuliwe ili Kiwanda cha Urafiki kirudi kwenye enzi za Mwalimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la bajeti ya usimamizi wa mazingira kwa kweli haiendani na kasi ya uharibifu wa mazingira. Katika hili naomba nimuunge mkono Mheshimiwa Waziri January, amezungumzia hapa kwamba Wabunge waliochangia ni watatu; jamani mazingira ndio uhai wa viwanda Tanzania, mazingira ndio kila kitu katika nchi yetu. Leo tunapoonyesha kwamba hatutambui mazingira tunawakatisha tamaa wataalam na tunaikatisha tamaa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba sasa Wabunge wajue kwamba bila ya mazingira hakuna viwanda, bila ya mazingira tunaharibu nchi yetu, mazingira tukiyahifadhi vibaya hata kilimo kitaharibika. Wabunge wapewe elimu zaidi Mheshimiwa Makamba waweze kutambua nini maana ya uhifadhi wa mazingira. Mheshimiwa January nakuunga mkono sana katika hili, sisi kama Kamati tumeridhika na kauli yako elimu bado ni ndogo hasa kwa Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba bajeti itengwe ya kutosha katika eneo la uhifadhi wa mazingira ili tuweze kudhibiti uharibifu unaoendelea. Uharibifu ni mkubwa sana kwenye migodi, viwanda, mito na vyanzo vya maji. Suala la tabianchi linatumaliza kwelikweli, kwa hiyo tunaomba sana haya mambo yote yaende pamoja lakini bajeti ni ndogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge ambao wamezungumzia haya, lakini Mheshimiwa Lema amezungumzia sana suala la Kiwanda cha General Tyre, General Tyre sisi kama Kamati tumelizungumza sana na zipo ahadi mbalimbali za Serikali. Sisi kama Kamati tunatilia mkazo zile ahadi za Serikali zifanyiwe kazi haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha General Tyre kinapoteza mapato, Watanzania wanakosa matairi bora, ajali barabarani ni nyingi na mara nyingi sana Kamati imejifunza mali zinazozalishwa Tanzania zina ubora wa hali ya juu. Bidhaa za ndani ya nchi yetu zina ubora wa hali ya juu ukilinganisha na bidhaa kutoka China, India na mataifa mengine. Kwa hiyo, Watanzania wanapenda sana bidhaa za ndani na tuendelee kuzisimamia ili Watanzania wapate kilicho bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mengine yamezungumzwa katika eneo hili, sisi tunaomba tuyatilie mkazo kwa maana ya haya yote sasa yafanyiwe kazi kwa hatua zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo pia tunaomba lifanyiwe kazi ni suala la gharama za uzalishaji. Suala la gharama za uzalishaji wataalam watusaidie, viwanda vya Tanzania vinaonekana gharama za uzalishaji zipo juu na kuna mifano hai kuanzia kwenye sukari, chuma, mabati na ndio maana leo mabati kutoka China yamezagaa Tanzania, wanasema ni mabati feki kwa sababu ni mabati ya bei nafuu. Gharama za uzalishaji ndani ya nchi yetu zimekuwa juu, tunaomba kikosi kazi cha wataalam wakishirikiana na Wizara ya Fedha walifanyie kazi hili ili tujue kuna tatizo gani, kuna shida gani katika eneo hili ili wale ambao wana viwanda waweze kusaidiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo jambo ambalo tunatakiwa sote kwa pamoja tulione na tulifanyie kazi. Vipo viwanda vilivyobinafsishwa leo vimekuwa ni viwanda vya mfano vinatoa gawio kubwa kwa Serikali. Kamati inashauri viwanda hivi vilindwe, mfano, viwanda vya sementi, viwanda vya sigara, viwanda vya mabati kama ALAF na viwanda hivi vyote vya bia kama Serengeti, TBL na hawa ambao wanatoa gawio ni viwanda ambavyo vimebinafsishwa pamoja na viwanda vya sukari vinavyofanya vizuri Serikali ikae na wadau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ilipotembelea wadau wana dukuduku, wadau wale wana mambo yao, tusipokaa nao tutawakatisha tamaa na gawio litashuka, uzalishaji utashuka na mapato ya nchi yatapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali yule ng’ombe anayetoa maziwa mengi tuendelee kumlea, tumpe majani mengi ili aendelee kutoa maziwa mengi, huo ndio wito wa Kamati. Pia wale ng’ombe ambao hawatoi maziwa, tuendelee kutafuta namna yoyote ya kuhakikisha na wale ng’ombe wanaendelea kutoa maziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kwa sababu viwanda vilivyobinafsishwa 156 asilimia 70 ya viwanda hivi vikifanya kazi, Taifa litapata ajira mapato ya nchi yataongezeka. Hapa Wabunge wengi wameshauri Mheshimiwa Spika aunde Kamati maalum ya kwenda kulisimamia hili na sisi kama Kamati tulisema hatuna tatizo na hilo, uamuzi ni uamuzi wa Spika. Kama inaundwa iundwe, tujue ukweli kwamba kuna nini katika jambo eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nimalizie kwa kusema kwamba zipo juhudi zinaendelea kufanyika na Kamati inaipongeza Serikali, zipo juhudi mbalimbali ambazo tayari tumeziona, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais anatekeleza kwa vitendo suala la Tanzania ya Viwanda. Kamati iko bega kwa bega na yeye na Kamati tutashirikiana na Serikali kuhakikisha kwamba tunasonga mbele kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa Bunge lako Tukufu lipitishe mapendekezo yetu ya Kamati kuwa azimio la Bunge kama yalivyoletwa na Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote naomba kutoa pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais kwa kumteua Profesa Muhongo kuwa Waziri wa Nishati na Madini; naomba nimwambie Mheshimiwa Waziri maneno ambayo yanazungumzwa aachane nayo, akaze buti tusonge mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi yake ambayo amefanya tumeiona, tuna matumaini makubwa na yeye. Labda niseme neno dogo katika eneo hili, niwaombe watendaji wanaomsaidia Mheshimiwa Waziri waoneshe mshikamano na upendo mkubwa kwa Waziri, wafanye kazi kama Waziri anavyofanya ili eneo hili sasa lisonge mbele. Wapo watendaji katika eneo hili inaonekana hawana speed ya Waziri mwenyewe. Niwaombe watendaji wa Wizara husika msaidieni Waziri, sisi Wabunge tuna imani naye, tusonge mbele, tulete maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala la umeme hususani umeme wa REA, vijijini. Naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri anaendelea kunipa ushirikiano wa kutosha katika yale maeneo ambayo huwa naonana naye na kuwasiliana naye.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu ambao unajitokeza katika mpango wa REA wa Awamu ya Pili. REA Wilaya ya Mvomero ipo kwenye tarafa zote nne. Na katika tarafa zote nne hizi kuna baadhi ya vijiji mradi ule unaendelea na baadhi ya vijiji mradi bado. Tumewasiliana mara nyingi na Msaidizi wa Waziri, tumewasiliana na Msofe wa REA, lakini bado yapo matatizo ya hapa na pale. Naomba Mheshimiwa Waziri aelewe kwamba, lile eneo la Kata ya Mtibwa, Wilaya ya Mvomero, katika Vijiji vya Kiduduwe, Kisara na Kunke, yule mkandarasi ambaye yuko pale leo ni miezi mitatu hajawalipa mafundi ambao wanafanya kazi ya kusambaza umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mafundi wale wapo zaidi ya 20 wanahangaika hawajalipwa na baadhi ya maeneo nguzo wameanza kuziondoa ambazo mwanzo walisambaza. Suala hili nilishamweleza Mheshimiwa Waziri , naomba hatua sasa zichukuliwe, lakini kuna maeneo ambayo umeme huu unasambazwa, ni maeneo ya barabarani peke yake, hakuna umeme unaokwenda vijiji vya ndani, umeme unalenga barabara kuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Langali kuna vijiji vitatu, umeme ubaki kijiji kimoja kitongoji kimoja; tunaomba Mheshimiwa Waziri atoe tamko, gharama ya kupeleka umeme Mgeta ni kubwa. Inakuwaje leo umeme unakwenda kijiji kimoja wakati mamilioni ya fedha yametumika? Mheshimiwa Waziri tunaomba atusaidie hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika eneo la Kibati, Kijiji cha Ng‟ai waliweka nguzo, wameziondoa, wanasema nguzo ni chache, sasa hivi wanaendelea kutafuta nguzo. Naomba Mheshimiwa Waziri atusaidie, ili ile azma yake na azma ya Serikali itimie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shida moja mbayo ipo, Mheshimiwa Waziri, wale ambao walipewa mkataba na REA na wao wame-subcontract kwa mafundi wengine na kampuni nyingine na wale ma-subcontractor na wao inaonekana uwezo ni mdogo. Tunaomba Serikali iliangalie hili, uwezo wa ma-contractor wanaopeleka umeme vijijini, hasa wale wanaopewa subcontract, uwezo wao ni mdogo.
Mheshimiwa Waziri, tunaomba eneo la Kibati, Mgeta, Turiani na sehemu za Mtibwa, watusaidie umeme ufike maeneo ambayo bado. Naomba ku-declare interest mimi ni mfanyabiashara wa mafuta naomba na mimi niseme mawili, matatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa leo tunaongelea mafuta ya petrol, mafuta ya kula wakati wake umeshapita. Naomba ku-declare interest na mimi ni mfanyabiashara wa mafuta ya petrol, ziko changamoto nyingi ambazo tunaona ni vyema tukazisema, ili Serikali izifanyie kazi. Changamoto ya kwanza, ni katika utaratibu mzima wa mafuta yanavyoagizwa, kwa maana ya bulk wale wanaoleta, sisi tunaunga mkono azma ya Serikali kuleta mafuta kwa utaratibu wa bulk, hilo mimi sina tatizo nalo na naliunga mkono.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ambalo lipo ni eneo ambalo mafuta yale yanaingia kwenye depot, kwa maana ya ghala. Sasa kwenye ghala unayatoa mafuta unayapeleka kwenye petrol station, hapo sasa ndipo ambapo tatizo linaanzia na EWURA lazima wajue changamoto hiyo. Sisi wengine hatuendi kule tunafanya utaratibu wa malipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wameongea na mimi naomba niseme. Tatizo lililopo ni kwamba, EWURA wao wanakwenda kumkaba moja kwa moja mlaji hawahangaiki na mpishi wa jikoni! Mpishi wa jikoni ni nani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpishi ni yule depot ambaye yeye ndiye amepata mafuta yale. Sasa yule mpishi, ambaye kapika chakula kile, wao hawahangaiki naye wanakwenda kuhangaika na mlaji na wanamsulubu sana mlaji! Naomba EWURA waliangalie hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya nyuma wakati wa Serikali ya Awamu ya Tatu utaratibu huu ulikuwa unasimamiwa na SGS, SGS walisumbua sana sekta hii. Mheshimiwa Rais Mkapa aliwatimua SGS na waliondoka kwa sababu walikuwa wanafanya mambo ambayo leo yanafanywa tena na EWURA; naomba Mheshimiwa Waziri aangalie matatizo ambayo yalikuwepo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikukabidhi gazeti hili uweze kulipeleka kunakohusika. Taarifa iliyotolewa humu ni taarifa ya TRA, afisa ambaye ametoa takwimu hizi anasema, leo kwenye Taifa letu fedha hizi zinapotea kwa sababu ya urasimu wa EWURA. Naomba sasa tubadilike, tubadilike katika eneo hili na wenzetu wa EWURA nao wabadilike, wabadilike ili tulete tija katika Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba niseme suala moja, TRA sasa hivi wao wanajua sehemu mbili ambazo zinapoteza mapato ya mafuta; sehemu ya kwanza ni transit, sehemu ya pili mafuta yanayokwenda ndani ya nchi, hususani kwenye migodi. Upande wa mafuta yanayokwenda kwenye migodi TRA wameweka monitored by track system.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana mafuta yanayokwenda migodini sasa hivi yako monitored tayari na yale ya transit yanalipiwa ushuru sasa hivi na wahusika wenyewe, sasa tunahangaika nini kama hayo mambo sasa hivi TRA wenyewe wanayashughulikia na wao wana-monitor mambo haya? Naomba EWURA wakae chini, waangalie upufungu wao, lakini wafike mahali waangalie na ubinadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapokifungia kituo cha mafuta unapoteza ajira za watu. Kituo kinafungwa mwaka mzima, yule mwenye kituo unampotezea mwelekeo wake, Serikali inakosa mapato, lakini yule uliyemfungia kituo ni mlalahoi au ni mjasiriamali anayehangaika kuuza mafuta rejareja, kwa nini usihangaike na wale wanaoshughulika na vinasaba? Usihangaike na wale wenye maghala ya mafuta? Kwa hiyo, wenzetu wa EWURA hebu liangalieni hili, mimi sina ugomvi na EWURA! Sina ugomvi kabisa na EWURA, lakini nawaomba changamoto zilizopo tuzifanyie kazi. Naomba sana changamoto zilizopo tuzifanyie kazi ili twende sambamba, wote nia yetu ni moja, tuhangaikie Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwambie Mheshimiwa Waziri, kuna suala la oil refinery ya Uganda kusafisha mafuta ghafi…
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Mvomero ni moja ya Wilaya ambazo zimekumbwa na tatizo kubwa sana la migogoro ya wakulima na wafugaji. Zipo juhudi mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ikiwemo Halmashauri ya Wilaya Mvomero, uongozi wa Mkoa na Serikali Kuu kupitia Wizara mbalimbali. Nia na madhumuni ni kuondoa au kupunguza migogoro hii, zipo changamoto nyingi sana tunazokabiliana nazo ikiwemo uhaba wa ardhi kwa wafugaji na kwa wakulima. Mbali na hilo, lipo tatizo la bajeti, fedha hazifiki kwa wakati katika mipango yetu kama Halmashauri ikiwemo kutenga maeneo ya malisho, majosho, kupima ardhi, barabara na maeneo ya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia lipo tatizo la watendaji wetu wa ngazi ya kijiji na kata, baadhi yao kupokea rushwa na kuongeza mgogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nieleze kuhusu hifadhi iliyopo Wilayani Mvomero ya Wami Mbiki. Hifadhi hii inaunganisha Wilaya za Morogoro Vijijini, Bagamoyo na Mvomero. Kwa upande wa Mvomero baadhi ya vijiji vimetoa ardhi yao kwa lengo la kuboresha hifadhi na pia kuongeza Pato la Taifa. Tatizo lililopo sasa ni uhaba wa ardhi kwa ajili ya ufugaji na kilimo. Ombi la wananchi, baadhi ya vijiji virudishwe kwa wananchi. Vijiji hivi vikirudi vitapunguza sana tatizo la migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa ndani ya hifadhi yapo makundi ya mifugo, wapo wakulima humo, yapo na makazi hewa. Tatizo kubwa ni kudorora kwa mipango ya uanzishaji wa hifadhi hii. Awali Serikali ilikuwa na nia ya dhati lakini hata wafadhili nao wamejitoa katika hifadhi na kukosa mwelekeo wa hifadhi hii. Ombi la wananchi ni kupewa maeneo yao ili wayaendeleze kwa kilimo na ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata makubaliano ya awali kati ya vijiji na hifadhi hayatekelezwi na hakuna faida inayoonekana. Watu wa maeneo ya hifadhi wanafaidika na makubaliano ya kuanzisha hifadhi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu shamba la mitiki Mtibwa, lipo Wilaya ya Mvomero, Tarafa ya Turiani. Ni shamba ambalo Serikali inapata mapato mengi licha ya wananchi kuwa walinzi wa amani wa shamba hili. Vijiji vina miradi ya maendeleo ya elimu, afya, maji, barabara na kadhalika. Tatizo hakuna mrabaha wanaopata wanakijiji wa maeneo ya jirani. Tunaomba Wizara kupitia idara yake, sasa itenge fungu la ujirani mwema ili kusaidia huduma za kijamii; hili litaleta na kudumisha mahusiano mema na pia kuongeza tija ya shamba. Pia tuna hitaji kubwa la madawati, Wizara iangalie uwezekano wa kutumia mabaki ya miti hii ya Mtibwa Teak kusaidia mabaki vijiji hivi vinavyozunguka shamba ili tupunguze tatizo la madawati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikumi National Park, inapatikana na Wilaya ya Mvomero, Kata ya Doma na Msongozi. Lipo tatizo kubwa sana la wanyama hususan tembo kuingia katika makazi na mashamba ya wananchi na kuleta athari kubwa sana ya mali na maisha ya wananchi wa Doma na Msongozi. Changamoto ni kubwa sana katika eneo hili. Wapo wananchi waliopoteza maisha yao, hadi sasa hakuna fidia iliyotolewa na TANAPA. Yapo mashamba na mali zilizoharibiwa hadi leo, hakuna fidia iliyolipwa na wanyama hawa wanatoka karika maeneo ya wananchi. Naomba kujua hatma ya malipo ya fidia za waathirika hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wananchi wa Doma na Msongozi ambao wapo mpakani na mbuga hii ya Mikumi wanahitaji madawati na kusaidia miradi ya maendeleo. Naomba TANAPA iwatupie jicho wananchi hawa katika mipango yao ya ujirani mwema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, Bodi ya Utalii iundwe na ije Mvomero, tunazo fursa nyingi za utalii kama vile milima ya Mgeta, maporomoko ya maji Bunduki ili maeneo haya yaingizwe katika sekta hii na yaweze kuchangia Pato la Taifa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi asubuhi hii ya leo na mimi naomba nianze kutoa pongezi nyingi na za dhati kabisa kwa Mawaziri wetu, Mheshimiwa Angellah, Mheshimiwa Jafo na Mheshimiwa Simbachawene kwa kazi kubwa na nzuri wanayofanya kulitumikia Taifa letu. Ni Mawaziri wasikivu, wachapakazi na mara nyingi ukipeleka shida zako wanakusikiliza na wanakuelewa. Hongereni na chapeni kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa anayofanya.
Mheshimiwa Rais amefanya mambo mengi makubwa, amerejesha nidhamu ya kutumia fedha na nidhamu kwenye ofisi za umma. Mheshimiwa Rais amethubutu kufanya mambo mazito kwenye reli, anga na barabara. Mheshimiwa Rais
amethubutu kulipa madeni ya nje na leo Serikali yetu inaanza kuaminika. Tuendelee kumuombea nmwenyezi Mungu ampe afya njema na mwenyezi mungu amuongezee ujasili aweze kulitumikia Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la Mvomero kwa upande wa elimu. Mvomero tuna upungufu wa walimu zaidi ya 200 kwenye shule zetu za msingi. Kabla sijaendelea naomba niseme kwamba walimu wa Mvomero walikuwa wanaida Serikali shilingi 137,000,000. Naomba niipongeze Serikali kwa kuleta fedha hizi na sasa hivi walimu wa Mvomero hawadai tena. Hongereni sana Mawaziri,
hongera sana Mheshimiwa Rais fedha zimekuja shilingi137,000,000 na walimu wote wamelipwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna upungufu wa walimu kama 200 tunaomba Serikali ituangalie kwa jicho la huruma.
Jiografia ya Mvomero imekaa vibaya, ukitoka Mvomero unakwenda mpaka Handeni unapakana na Mkoa wa Tanga na Kilindi, unarudi mpaka kwenye mbuga za wanyama za Mikumi, unakwenda mpaka na Chuo Kikuu cha Mzumbe na unapanda mpaka kwenye milima ya Mgeta unapakana tena na tarafa nyingine za Morogoro Vijijini. Jiografia ya Mvomero imekaa vibaya, naomba Waheshimiwa Mawaziri tuangalie
ni jinsi gani Mvomero tunaweza kuigawa aidha katika Halmashauri mbili au katika majimbo mawili. Mvomero imekaa vibaya tunatumia muda mwingi sana kutembea kupeleka huduma, naomba Serikali iliangalie hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika Wilaya ya Mvomero tuna tarafa nne lakini tuna sekondari mbili za Alevel.
Tunaomba Serikali itusaidie fedha ambazo tumeomba zile tarafa mbili zilizobaki tuweze kupata sekondari za A-level. Tarafa za Turiani na Mvomero zinazo shule hizo, lakini tarafa viongozi mtusikie katika hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la TASAF kwa ufupi kabisa. Fedha za TASAF zinazokuja katika zoezi la kusaidia kaya maskini zinakwenda muda mbaya.
Wataalam wetu wanatoka na fedha benki jioni saa kumi, wanatembea kwa zaidi ya saa mbili/tatu wanafika usiku, wananchi wengine wanakuwa wameshapata vinywaji wamechangamka kunakuwa na vurugu. Naomba Waziri, dada yangu Mheshimiwa Angellah uliangalie hilo na utoe maelekezo na waraka kwamba fedha zipelekwe muda wa mchana na muda mzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la zahanati na afya. Mheshimiwa Waziri Wilaya ya Mvomero tuna upungufu mkubwa sana wa huduma ya afya. Tumejenga Hospitali ya Wilaya, jengo limekamilika lakini bado umeme. Bajeti ambayo wataalamu wetu waliiandaa tunahitaji shilingi 100,000,000 tuweze kuifungua hospitali ile ya Wilaya na fedha hizi tayari tumeziomba. Naomba Mawaziri mnaohusika muweza kutuidhinishia fedha hizo tuweze kufungua Hospitali ya Wilaya ya Mvomero. Nawaombeni sana fedha zilizotumika ni nyingi, idadi ya fedha iliyobakia ni ndogo, tunaomba bajeti ile idhinishwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuna Hospitali Teule inaitwa Turiani Hospitali. Hospitali ile wananchi ambao wanakwenda kupata huduma pale wanapata huduma kwa gharama kubwa. Hospitali ile haitusaidii chochote wananchi wa Mvomero. Fedha ambazo zinapelekwa bado hazisaidii, wananchi wanatozwa gharama mbalimbali na taratibu hazifuatwi. Huduma wanazopata mama na mtoto bado wanatozwa na sera ya Serikali inasema huduma ya mama na mtoto ni bure. Mheshimiwa Jafo uliniahidi kwamba tutakwenda pamoja Mvomero, naomba tekeleza ahadi yako, tukimaliza Bunge hili au Jumamosi moja chapa kazi twende zetu ukaone matatizo yaliyopo na uweze kutushauri na kutusaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo naomba niliseme, Wilaya ya Mvomero imebarikiwa ina mito mingi, maji mengi na ardhi nzuri sana. Tuna green land kubwa sana Mvomero. Wabunge karibuni, chukueni mashamba mlime.
Tatizo letu tunahitaji tusaidiwe na Serikali ili kilimo kile kiwe kilimo cha kisasa tuweze kupata fedha za kutusaidia baadhi ya maeneo tuweze kumwagia zaidi tuweze kuyatumia yale maji vizuri. Fursa kubwa ipo tatizo ni fedha tunazoomba haziletwi kwa wakati na zinakuja fedha ndogo. Naomba sana fedha hizo zije kwa wakati ziweze kutusaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho kabisa na naona muda unakwenda, tunaomba sana Idara ya Ujenzi Mvomero inayoshughulikia barabara haina gari kufuatilia miradi ya barabara. Mheshimiwa Jafo tuliongea jambo hili ukaniambia tutakaa chini tutazungumza. Naomba kupitia bajeti ya Wizara yenu, Mvomero jiografia yake imekaa vibaya, tunaomba gari Idara ya Ujenzi tuweze kufuatilia barabara zetu tuweze kuleta maendeleo kwa Mvomero yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni na naunga mkono hoja mia kwa mia.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi jioni ya leo na mimi pia niweze kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaendelea, kwa kuwa nina mambo mengi ya kusema, naomba nitamke kabisa kwamba naunga mkono kwa asilimia mia kwa mia bajeti hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumpongeza sana sana Mheshimiwa Rais wetu. Mheshimiwa Rais amethubutu na ameweza kufanya mambo makubwa na mazito katika sekta ya barabara, anga, reli na bandari. Mheshimiwa Rais amefanya mambo mengi sana kwenye sekta hiyo na ameendelea kufanya mambo mengi katika maeneo mbalimbali na katika Jimbo langu la Mvomero kulikuwa na barabara ya lami ambayo ilikuwa imesimama kwa miaka mitano.
Mheshimia Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alipokuja mwaka 2015 kuomba kura kama mgombea, alitamka iwapo atachaguliwa kuwa Rais, barabara ile itawekwa lami. Na kweli ujenzi umeanza mwaka 2016 lami ile imeshakamilika kwa kilometa 40 bado kilometa nane zimebaki, tuna mategemeo mwezi wa nane wa tisa itakuwa imekamilika. Kwa mazuri yote haya anayofanya Mheshimiwa Rais ndani ya nchi yetu na ndani ya Wilaya ya Mvomero, Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako naomba nimpigie salute Mheshimiwa Rais. Nampigia salute ya heshima, nampigia salute ya upendo, Mwenyezi Mungu ampe imani zaidi, ampe afya njema aendelee kuliongoza Taifa letu. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Engineer Mfugale, Engineer wa TANROADS Mkoa Morogoro Mama yetu Engineer Mtenga, kwa kazi kubwa wanayofanya katika kusimamia masuala yote ya barabara katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na reli. Serikali yetu sasa hivi ina mpango wa kujenga reli na mpango ule umeanza na reli ile itakuwa reli ya kisasa, reli ya kasi ambayo tayari imezinduliwa kwa awamu ya Morogoro - Dar es Salaam - Morogoro. Nimuombe Mheshimiwa Waziri, niwaombe na wataalam, reli ile inapoanza kazi kuja Morogoro na kwenda mikoa mingine, kwa kuwa itakuwa ni reli ya kasi, abiria wengi watapanda, ile miundombinu iliopo leo katika miji ya Morogoro na miji mingine haitoshelezi mahitaji ya kisasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri wewe na wataalamu wako, jaribuni kubuni mkakati wa kuweka miundombinu mingine, tuseme mfano reli imepakia abiria 1000, abiria 1000 wanaoshuka katika reli ile katika kituo cha leo cha Morogoro kutakuwa na msongamano mkubwa, magari yatakuwa mengi kuwapeleka wale vituo vya mabasi na maeneo mengine. Jaribuni kujenga vituo vipya vitakavyokidhi mahitaji ya reli ya kisasa. Huo ni ushauri wangu kwa Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nirudi kwenye barabara ya lami inayojengwa kutoka Magole - Turiani - Mziha
- Handeni. Barabara hii lengo lake kubwa ni kufungua milango ya uchumi kutoka Tanga - Mombasa - Arusha - Kilimanjaro na maeneo mengine. Na kwa lugha njema barabara hii ndiyo barabara mbadala kwa barabara ya Chalinze - Segera. Lolote litakalokea kwenye Daraja la Wami, ujue barabara mbadala ni barabara hii ya Turiani - Mziha - Handeni. Kipande cha Magole - Turiani kinakaribia kukamilika, kipande cha kutoka Turiani - Mziha – Handeni, Mheshimiwa Waziri nikuombe mkandarasi yuko site, ana mitambo ya kisasa, ana uwezo mkubwa, na wewe kutambua uwezo wake na wataalam wako mkandarasi yule umempa kujenga interchange ile ya Ubungo. Mkandarasi huyu ndio anajenga pale Ubungo ambae leo anajenga lami Turiani, kwa sababu ana uwezo ana vifaa ana mtaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri, Engineer Mfugale na wengine wote wa TANROADS, kazi yake mmeiona, hebu muachieni amalize kile kipande kilichobaki, Serikali itaokoa mamilioni ya fedha. Hakuna mobilization, hakuna chochote zaidi ya yule kupewa kazi na kuendelea na barabara. Na barabara ile ndiyo itakuwa barabara mbadala kwa baadaye. Lakini leo Tanga tunajenga bomba la mafuta toka Uganda kuja Tanga, wenzetu wa Uganda watasafirisha mafuta yao kupitia kwenye meli. Tanzania tukinunua mafuta yale tutayasafirisha aidha kwa reli au kwa barabara. Barabara ya Segera - Chalinze ina msongamano. Mheshimiwa Waziri elekeza nguvu Handeni - Mziha - Turiani kupitia Dumila. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo naomba niseme suala la barabara za Halmashauri za Wilaya ya Mvomero ambazo tumeziomba zipandishwe daraja na ninaomba niseme kwamba taarifa nilizonazo kila Mkoa kuna barabara zimepandishwa daraja. Barabara iliyopandishwa daraja ya Mvomero kutoka Langali - Nyandila kwenda Kikeo, naomba sasa barabara ile itengewe fedha mwaka huu. Tusisubiri kwa sababu imepanda daraja mwaka huu isubiri bajeti ya mwakani. Na kila mkoa wamepata barabara, kila mkoa kuna barabara zimepanda daraja.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mikoa yote na Wilaya zote fedha zianze mwaka huu. Kwa sababu tunakiu ya barabara hizi zipande daraja naomba fedha hizi sasa zitolewe mwaka huu na barabara zile zianze kazi mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, Meneja wa TANROADS Morogoro aliandika barua kwa Wizara yako kukumbushia ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alipofanya ziara Mvomero katika tTarafa ya Mgeta, kwamba barabara ya kutoka Chuo Kikuu Mzumbe kwenda Mgeta itawekwa lami. Mheshimiwa Waziri, nakuomba wewe na timu yako tukumbukane katika ahadi ile ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niende kwenye mawasiliano. Mheshimiwa Waziri wewe ni shahidi, nimekuja kwako mara nyingi, Mheshimiwa Naibu Waziri ni shahidi tumezungumzia minara kwa ajili ya Mvomero. Halotel wamefanya kazi nzuri, wamejenga minara katika baadhi ya maeneo, lakini maeneo yafuatayo bado tuna upungufu wa minara. Maeneo ya kata za Pemba, Kinda, Mascut, Homboza pamoja na kata ya Kikeo pale Mgeta.
Mheshimiwa Waziri nakuomba sana waelekeze wenzetu wa Halotel na mitandao mingine waweze kutukamilishia ahadi ya mitandao hii ili wananchi waweze kufanya biashara zao, waweze kupata huduma mbalimbali kupitia simu za mkononi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho. Nimeona kuna bajeti imetengwa kwa ajili ya barabara ya Msamvu – Bigwa. Unapozungumza Msamvu – Bigwa unazungumzia Manispaa ya Morogoro, unazungumzia barabara ya Morogoro Mjini. barabara ya Morogoro Mjini sasa hivi ina msongamano mkubwa wa magari.
Nawaomba sana wenzetu wataalamu, barabara ile wachore ramani ya two way, kwa sababu ya reli inayokuja na kituo kile kilichopo barabara ile ina msongamano mkubwa. Fedha zilizotengwa wataalamu waelekeze kutoka Msamvu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi asubuhi ya leo. Na mimi naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na wataalam wao, lakini salamu za kipekee kwa Mheshimiwa Waziri, amefanya kazi kubwa sana katika Mkoa wa Morogoro na Wilaya ya Mvomero. Mheshimiwa Waziri kazi uliyofanya Morogoro ni ya historia, migogoro ya ardhi imepungua, migogoro ya wakulima na wafugaji inaendelea kupungua. Tunaomba jicho lako la huruma liendelee kutusaidia wananchi wa Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nielekeze matatizo yafuatayo kwa sababu muda wenyewe ni mdogo. Mheshimiwa Waziri, suala la kwanza tuna mgogoro wa mipaka ya kiutawala kati ya Manispaa ya Morogoro na Wilaya ya Mvomero, huu mgogoro ni mkubwa sana, naomba sana utusaidie. Halmashauri ya Mvomero imeanzishwa kwa GN yake, Manispaa ina GN yake, lakini tunaomba sasa hivi

Mheshimiwa Waziri, Ofisi yako, wataalam wako waje watoe tafsiri ya GN. Mgogoro unazidi kuendelea, mipaka inaingiliana na wananchi wa Mvomero wanakosa haki kwasabbau Manispaa wanaingilia eneo la Mvomero na wanaanza kugawa ardhi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba kauli ya Serikali katika suala hili na tunaomba sana uje utusaidie Mkuu wa wilaya, wataalam wa Mvomero na wananchi pia tumeanza zoezi hili lakini halina mafanikio kwa sababu tunahitaji nguvu kubwa ya Serikali.

Mheshimiwa Waziri, jambo la pili ambalo ningependa sana kulizungumza kwa sababu ya muda nao unakwenda ni kuhusu ardhi kubwa. Mvomero kuna ardhi ambazo hazijaendelezwa, kuna ardhi inaitwa Katenda Group hawa wana heka 12,500 tangu mwaka 2002 mpaka leo ardhi haijaendelezwa. Mheshimiwa Waziri tunaomba ofisi yako sasa itusaidie kutupatia ardhi hii ili wananchi wa Mvomero na Watanzania wengine waweze kufaidika na ardhi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu Mheshimiwa Waziri ni upungufu wa wataalam. Mvomero tuna upungufu mkubwa wa wataalam. Nimpongeze Mheshimiwa Rais amevunja CDA, wataalam wa CDA nawakaribisha Mvomero. Tusaidiane wataalam waje Mvomero, tunahitaji baadhi ya wataalam katika maeneo yafuatayo. Tunahitaji Maafisa wa Mipango Miji wawili waaminifu, huo ndiyo upungufu wetu wa kwanza, wa pili tunahitaji Mthamini, na Mrasimu wa Ramani. Tunaomba Mheshimiwa Waziri kwa kuwa haya mambo mengine nitakuwa nayo kwa maandishi nitakuletea, tunaomba tupate watumishi hawa ili Mvomero sasa isonge mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne ni kutopata gawio la asilimia 30. Mvomero tunadai zaidi ya shilingi milioni 178, gawio hili hatujalipata bado. Mheshimiwa Waziri, kuna ahadi za Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa William Lukuvi alizozitoa Mvomero. Naomba kuzitaja ahadi zake, ahadi ya kwanza aliahidi kutuletea vifaa vya upimaji (RTK) vifaa hadi leo Mvomero hatujavipata. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunaomba utusaidie ahadi yako, tekeleza, tuletee vifaa vya upimaji. Ahadi ya pili tunaomba kukamilisha uandaaji wa mipango na matumizi ya ardhi kwa vijiji 52 kati ya vijiji 130. Ahadi ya tatu Mheshimiwa Waziri tunaomba ukamilishaji wa upimaji wa mipaka ya kiutawala vijiji 32 kati ya vijiji 130. Mheshimiwa Waziri tunaomba sana utusaidie vifaa vya upimaji ili Mvomero tusonge mbele zaidi na zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mvomero hatuna ofisi ya ardhi, tunatumia ofisi ya Idara ya maji. Sasa umetoa ofisi tatu na unaendelea na mipango mizuri kwa maeneo mengine Mvomero umeisahau, tunaomba kwenye mipango yako mizuri uweze kutusaidia ili na sisi tuwe na ofisi ya ardhi. Mwisho ni kuhusu Ofisi ya Kanda ya Mashariki ambayo baada ya kutoa tamko rasmi sasa kwamba Kanda ya Morogoro inaondoka na badala yake tunahamia huku Dodoma. Mheshimiwa Waziri kwanza nikupongeze ulianzisha Kanda mwaka 2015, ukajenga ofisi nzuri Morogoro, ofisi imefanya kazi nzuri wananchi wa Mikoa ya Pwani na Morogoro wamepata Hati zaidi ya 5,000; sasa kuondoa Kanda leo na kuturudisha tena Dodoma kwa kweli naona unaturudisha nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri masuala yangu mengine nikuletee kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi asubuhi ya leo. Na mimi naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na wataalam wao, lakini salamu za kipekee kwa Mheshimiwa Waziri, amefanya kazi kubwa sana katika Mkoa wa Morogoro na Wilaya ya Mvomero. Mheshimiwa Waziri kazi uliyofanya Morogoro ni ya historia, migogoro ya ardhi imepungua, migogoro ya wakulima na wafugaji inaendelea kupungua. Tunaomba jicho lako la huruma liendelee kutusaidia wananchi wa Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nielekeze matatizo yafuatayo kwa sababu muda wenyewe ni mdogo. Mheshimiwa Waziri, suala la kwanza tuna mgogoro wa mipaka ya kiutawala kati ya Manispaa ya Morogoro na Wilaya ya Mvomero, huu mgogoro ni mkubwa sana, naomba sana utusaidie. Halmashauri ya Mvomero imeanzishwa kwa GN yake, Manispaa ina GN yake, lakini tunaomba sasa hivi Mheshimiwa Waziri, Ofisi yako, wataalam wako waje watoe tafsiri ya GN. Mgogoro unazidi kuendelea, mipaka inaingiliana na wananchi wa Mvomero wanakosa haki kwasabbau Manispaa wanaingilia eneo la Mvomero na wanaanza kugawa ardhi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba kauli ya Serikali katika suala hili na tunaomba sana uje utusaidie Mkuu wa wilaya, wataalam wa Mvomero na wananchi pia tumeanza zoezi hili lakini halina mafanikio kwa sababu tunahitaji nguvu kubwa ya Serikali.

Mheshimiwa Waziri, jambo la pili ambalo ningependa sana kulizungumza kwa sababu ya muda nao unakwenda ni kuhusu ardhi kubwa. Mvomero kuna ardhi ambazo hazijaendelezwa, kuna ardhi inaitwa Katenda Group hawa wana heka 12,500 tangu mwaka 2002 mpaka leo ardhi haijaendelezwa. Mheshimiwa Waziri tunaomba ofisi yako sasa itusaidie kutupatia ardhi hii ili wananchi wa Mvomero na Watanzania wengine waweze kufaidika na ardhi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu Mheshimiwa Waziri ni upungufu wa wataalam. Mvomero tuna upungufu mkubwa wa wataalam. Nimpongeze Mheshimiwa Rais amevunja CDA, wataalam wa CDA nawakaribisha Mvomero. Tusaidiane wataalam waje Mvomero, tunahitaji baadhi ya wataalam katika maeneo yafuatayo. Tunahitaji Maafisa wa Mipango Miji wawili waaminifu, huo ndiyo upungufu wetu wa kwanza, wa pili tunahitaji Mthamini, na Mrasimu wa Ramani. Tunaomba Mheshimiwa Waziri kwa kuwa haya mambo mengine nitakuwa nayo kwa maandishi nitakuletea, tunaomba tupate watumishi hawa ili Mvomero sasa isonge mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne ni kutopata gawio la asilimia 30. Mvomero tunadai zaidi ya shilingi milioni 178, gawio hili hatujalipata bado. Mheshimiwa Waziri, kuna ahadi za Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa William Lukuvi alizozitoa Mvomero. Naomba kuzitaja ahadi zake, ahadi ya kwanza aliahidi kutuletea vifaa vya upimaji (RTK) vifaa hadi leo Mvomero hatujavipata. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunaomba utusaidie ahadi yako, tekeleza, tuletee vifaa vya upimaji. Ahadi ya pili tunaomba kukamilisha uandaaji wa mipango na matumizi ya ardhi kwa vijiji 52 kati ya vijiji 130. Ahadi ya tatu Mheshimiwa Waziri tunaomba ukamilishaji wa upimaji wa mipaka ya kiutawala vijiji 32 kati ya vijiji 130. Mheshimiwa Waziri tunaomba sana utusaidie vifaa vya upimaji ili Mvomero tusonge mbele zaidi na zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mvomero hatuna ofisi ya ardhi, tunatumia ofisi ya Idara ya maji. Sasa umetoa ofisi tatu na unaendelea na mipango mizuri kwa maeneo mengine Mvomero umeisahau, tunaomba kwenye mipango yako mizuri uweze kutusaidia ili na sisi tuwe na ofisi ya ardhi. Mwisho ni kuhusu Ofisi ya Kanda ya Mashariki ambayo baada ya kutoa tamko rasmi sasa kwamba Kanda ya Morogoro inaondoka na badala yake tunahamia huku Dodoma. Mheshimiwa Waziri kwanza nikupongeze ulianzisha Kanda mwaka 2015, ukajenga ofisi nzuri Morogoro, ofisi imefanya kazi nzuri wananchi wa Mikoa ya Pwani na Morogoro wamepata Hati zaidi ya 5,000; sasa kuondoa Kanda leo na kuturudisha tena Dodoma kwa kweli naona unaturudisha nyuma.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri masuala yangu mengine nikuletee kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi asubuhi ya leo. Niungane na Wabunge wenzangu kukukaribisha tena Bungeni karibu sana Bungeni tumefarijika sana kukuona ukiwa na afya njema na unang’ara kweli kwenye Kiti chako, Mwenyezi Mungu akufanyie wepesi zaidi, Inshallah. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi asubuhi ya leo na mimi niweze kuzungumza mawili matatu ya maendeleo kwa nchi yetu na Wilaya yetu ya Mvomero.

Naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa anayofanya katika nchi yetu, kwa kazi ambayo italeta manufaa makubwa leo na kesho na kesho kutwa tunampongeza sana na tunasema wananchi wa Mvomero tuko naye bega kwa bega.

Mheshimiwa Spika, pia naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi ambayo anafanya hususani kusimamia masuala mbalimbali ya pamba, kilimo na maendeleo kwa ujumla na naomba niwapongeze na wenzake wote na timu yao yote.

Mheshimiwa Spika, bila ya kupoteza muda naomba nizungumzie suala la Wilaya ya Mvomero, uvamizi wa ardhi katika Wilaya ya Mvomero uliofanywa na Manispaa ya Morogoro, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, Waziri wa TAMISEMI, Waziri wa Maliasili na Waziri wa Ardhi kwa pamoja wanisikilize kwa makini sana.

Mheshimiwa Spika, Manispaa ya Morogoro imevamia eneo la Wilaya ya Mvomero na wameanzisha mitaa miwili ndani ya Wilaya ya Mvomero, mtaa wa kwanza unaitwa CCT Forest na mtaa wa pili unaitwa Maili Kumi na Nane.

Mheshimiwa Spika, Mitaa hii ipo ndani ya Wilaya ya Mvomero wapiga kura wa Mjini wanapiga kura katika Wilaya ya Mvomero na maeneo hayo yalianzishwa kwa mujibu wa utaratibu na sheria za nchi yetu. GN. No. 204 ya mwaka 1953 ilianzisha msitu wa kuni ambao uko ndani ya Wilaya ya Mvomero. GN No. 366 ya mwaka 2002 ilianzisha Wilaya ya Mvomero na GN Na. 242 ya mwaka 1991 ilianzisha Manispaa ya Morogoro hizi GN zote zipo kisheria na zipo pale kila mmoja inaeleza mipaka na maeneo jinsi yalivyo. Nimuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu, nimuombe Waziri wa TAMISEMI mara watakapofanya majumuisho naomba tamko la Serikali eneo hili sasa litambulike kama eneo halali la Wilaya ya Mvomero na wavamizi wote waondoke wananchi waliopo maeneo yale tutawatambua kama wananchi wa Mvomero hatuna ugomvi nao. Kwa hiyo, naomba suala hili lifanyiwe kazi na Serikali na tupate majibu ya haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni eneo la NARCO - National Ranch zile kubwa ambazo ziligawiwa kuna eneo ambalo walipewa wenzetu ambao hadi leo maeneo yale hawajaendeleza kuna kampuni mbili moja inaitwa Katenda group na moja inaitwa Elisa Mollel walipewa heka 5000. Eneo lile walipewa mwaka 2002 hadi leo maeneo yale hawajayaendeleza, leo kuna kaya zaidi ya 430 zinaishi eneo lile, naomba Waziri muhusika aunde timu yake waje wakague eneo lile watukabidhi Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero, tuweze kuliendeleza, tuweze kuwaleta wawekezaji eneo limekaa bure limekuwa pori yamebaki majoka, yamebaki mapori ambayo hayana faida yoyote kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na muda unavyoenda haraka naomba haya maeneo yote ya NARCO yaliyopo ndani ya Wilaya ya Mvomero Mheshimiwa Waziri alikuja akazungumza naomba sasa aje na timu yake tukae na timu ya Mvomero tuweze kuona ni namna gani maeneo yale yataendelezwa na yataleta faida.

Mheshimiwa Spika, Mvomero tumepata wawekezaji wengi maeneo ya barabarani yote ni mapori hayaendelezwi, namuomba Waziri wa Maliasili akumbuke ombi la Wilaya ya Mvomero tuliloandika barua na kupeleka ofisini kwake tunahitaji heka 10,000 za barabarani tuwape wawekezaji waweze kujenga viwanda, waweze kuleta mashamba bora ya kisasa tuweze, kusonga mbele. Kwa hiyo, naomba Waziri wa Maliasili aweze kukumbuka barua yetu ya Mvomero.

Mheshimiwa Spika, pia tuna mgogoro wa hifadhi na Mikumi National Park na kijiji cha Doma na Kata ya Doma, namuomba Waziri wa TAMISEMI, Waziri wa Maliasili, Waziri wa Ardhi watuletee timu tuweze kukaa nao chini Mikumi National Park wameingia kwenye eneo la Mvomero, wameingia kwenye mashamba ya wakulima na sasa hivi wameweka na beacon, suala hili naomba tamko litolewe na ikiwezekana timu ya Mawaziri tukutane tuweze kuona tunafanyaje.

Mheshimiwa Spika, lakini naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu atoe tamko kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero, mapato ya ndani asilimia 40 na ile 20 asilimia 60 mapato ya ndani yale yaende kwenye miradi ya wananchi, fedha za mapato ya ndani zinatumika kulipa madeni ya Halmashauri, fedha za mapato ya ndani zinatumika katika mipango ya Wilaya ambayo sio maendeleo na miradi ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, wananchi wamejenga zahanati wanahitaji bati, wananchi wanahitaji pampu ya kisima fedha hizi zinakwenda kwenye sherehe za Nane Nane, fedha hizi zinakwenda kwenye mambo mengine, naomba tamko la Waziri Mkuu fedha za mapato ya ndani kwa mujibu wa kanuni na sheria zirudi kwenye miradi ya wananchi na bahati nzuri Waziri Mkuu nimeonana nae na baadaye tutaonana nitamkabidhi na baadhi ya documents ili tamko litolewe wananchi wa Mvomero wapate maendeleo kutokana na mapato ya ndani.

Mheshimiwa Spika, lipo tatizo moja kubwa katika Wilaya ya Mvomero, Wilaya ya Mvomero kijiografia unatoka mpakani na Handeni unarudi mpaka Morogoro Mjini unaanza safari unaacha Manispaa unakwenda Mzumbe, unakwenda mpaka Mgeta, unakwenda mpaka Kikeo, unasafiri masaa zaidi ya 10 kutoka kwenye Kata moja kwenda kwenye Kata nyingine tulipeleka ombi tunaomba Jimbo la Mvomero ligawanywe ili tuwe na Majimbo mawili ya uchaguzi. Suala hili tumelifikisha kwenye vikao mbalimbali bado tutaleta na documents zetu tunaomba Serikali inapofanya marekebisho ya Majimbo ya Uchaguzi watuangalie Mvomero namna gani jiografia yetu ilivyokuwa ngumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho naomba kuipongeza Serikali, ninampongeze Waziri wa Utumishi kwa kauli yake ya leo Bungeni kuhusu ajira za watumishi hii ndiyo Serikali sikivu ya CCM, Waziri wa Utumishi nakupongeza, naipongeza Serikali kwa maamuzi haya mazuri ambayo yana tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, bila ya kupoteza muda nasema naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana asubuhi ya leo na mimi kunipatia nafasi niweze kuchangia mawili, matatu katika bajeti hii ya Tanzania kwa mwaka 2018/2019. Naomba niseme naunga mkono hoja asilimia mia kwa mia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kusema, sasa hivi tuna kaulimbiu ya Tanzania ya Viwanda. Katika kauli mbiu hii naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais anaisimamia kauli yake hii kwa vitendo. Sisi kama Kamati ya Viwanda na Biashara tulipata changamoto mbalimbali za wadau katika maeneo mbalimbali. Katika bajeti ya mwaka huu, naomba nimpongeze sana Waziri wa Fedha changamoto nyingi zimefanyiwa kazi na Serikali, zimefanyiwa kazi na TRA kwa maana hiyo Rais wetu anatekeleza kwa vitendo kauli yake ya Tanzania ya Viwanda. Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na TRA wote nawapongeza sana kwamba sasa tunakwenda vizuri sana katika eneo hili la Tanzania ya Viwanda.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naanza na suala hili la electronic stamp. Naunga mkono hoja, sina matatizo kwani mapato yataongezeka, uhakiki wa uzalishaji utafanyika lakini wasiwasi wangu ni eneo moja la gharama. Kampuni ambayo mnaingia nayo ubia TRA na Serikali kuna viwango wameeleza, kuna dola 6, 10 na 13. Unapozungumzia dola 6 unazungumzia soft drinks, unapozungumzia dola 10 unazungumzia alcohol, unapozungumzia dola 13 unazungumzia spirit, sigara na vitu vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu haina coins ya Sh.10, 20 au 30, tuna coins ya Sh.50 na 100 ambazo nazo ni chache sana. Mimi ni mdau nina Super Market, tuna shida kubwa sana ya coins ya Sh.100 na 200. Leo tunaposema dola 6, huyu bwana atanunua stamp Sh.1,000 atazalisha chupa 1,000, ina maana kila chupa moja imepanda Sh.13. Soda leo inauzwa Sh.500 kwa kutumia utaratibu wa electronic stamp, anatakiwa auze Sh.513, tunapata wapi coins Sh.13? Maana yake ni kwamba wafanyabiashara watauza Sh.550, ile stamp sasa itatoka Sh.13 ya ukweli itakwenda kwenye Sh.50. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye bia wanasema dola 10 sawasawa na Sh.23. Hatuna coins ya Sh.23, atatoka kwenye Sh.23 ataenda kwenye Sh.50 kwa maana stamp sasa pale ni Sh.50. Naomba TRA na Serikali mlifanyie kazi hili, gharama ziko juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba kidogo niulize swali, je, wakati mna-bargain na hii kampuni, mliwaeleza ukweli wa uzalishaji wa volume za chupa Tanzania? Leo tunazalisha chupa zaidi ya bilioni 10 za soda, juisi, bia na vinywaji mbalimbali, viwanda vimekuwa vingi. Unapofanya biashara na mtu unatakiwa ufanye bargain, volume ya bilioni 10 chupa si volume ndogo. Kama ni dola 6 lazima wapunguze wafanye dola 2 au 3, volume ni kubwa sana ya hizi chupa.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, TRA walikwenda na volume halisi? Walifanya uhakiki kwenye viwanda? Mbona wenye viwanda wanasema hawajafanya uhakiki huo au uhakiki wanatumia uwakilishi wa return zao kwenye TRA? Kama wanatumia uwakilishi wa return za TRA bado liko tatizo. Kwa sababu kuna viwanda vinazalisha lakini hawapeleki return za ukweli TRA, wanadanganya na Kamati tuliwashauri wafanyabiashara wawe wakweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi kwenye upande wa ETS (Electronic Tax Stamp) sina tatizo. Tatizo langu hizo gharama ambazo zipo mwisho zitamwangukia mlaji, Tanzania hatuna coins hesabu zake tutazifanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa mashine za EFD tumeanza kupata matatizo. Mwezi mmoja nyuma server iliharibika, wafanyabiashara siku nne, tano tulishindwa kupelekea returns reports zetu matokeo yake mapato kidogo yalipungua. Hata leo napozungumza mimi hapa bado ile server haijakaa sawa, EFD bado inasumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha amefanya juhudi kubwa, mimi na Mheshimiwa Ndassa tulimwona na tulimpa na ushahidi na tunawasifu sana na Naibu Waziri walifanya kazi kubwa lakini bado server ya EFD haijatengemaa, je, imehujumiwa? Leo Mheshimiwa Waziri ameondoa kodi ya EFD, je, server iko sawasawa? Kama kwenye EFD mashine ndogo hizi tunachemka, je, kwenye electronic stamp tutakuwa na hali gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ushauri wangu tuangalie upande wa gharama. Naunga mkono, itaongeza mapato, itafanya uhakiki, hatutaibiwa lakini tunali-handle vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye eneo la pili la industrial sugar. Sisi Kamati yetu ya Viwanda tulipata malalamiko mengi kuhusu refund ya VAT na ile ya 15%. Wafanyabiashara ambao ni Big Five: Cocacola Kwanza Pepsi, Azam, Nyanza Bottlers na Bonite wanaidai Serikali zaidi ya shilingi bilioni 35. Fedha hizi ni mitaji yao ya ndani, hawajapata ile return yao ya 15%. Kamati imewashauri waendelee kuvumilia, Serikali inalifanyia kazi suala lao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika eneo hilo, nia ya Serikali ya kudhibiti watu ambao si waaminifu ni njema, ndiyo maana tunawatoza 15% . Sasa tubadilike, badala ya kutoza 15% tuweke penalt, faini ambazo zitasababisha Serikali kupata mapato ya moja kwa moja. Hizi fedha si zetu ni zao, tunatakiwa tufanye refund. Tuweke audit team maalum, kila miezi mitatu iende kwenye viwanda hivi ihakiki Industry sugar imetumika kiasi gani, industry sugar ambayo haikutumika viwandani, wapigwe faini na penalt na ikiwekana wakirudia makosa wafutiwe leseni. Kwa utaratibu huu wa kuchukua refund zao tunawanyima mitaji yao. Leo mitaji mingi imelala Serikalini na wanalalamika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niingie eneo la kilimo (agri- business), nazungumizia kilimo cha biashara. Tanzania tuna eneo kubwa na ardhi nzuri sana, maji ni mengi lakini bado Serikali haijawapanga wananchi na wakulima wake waingie kwenye agri-business. Leo nenda Dubai wana kila aina ya matunda duniani lakini wale supplier wanafanya packaging nzuri, wanaweka matunda yao katika hali ya usafi wanafanya export. Matunda ya Dubai yanatoka Malaysia, Indonesia, India ns Vietnam. Embe linatoka maeneo ambayo maembe ya Tanzania ni mazuri zaidi. Twende kwenye agri- business tuwahamasishe watu wetu ili tusonge mbele zaidi. Katika maeneo ambayo yana ardhi nzuri, rutuba nzuri, mfano Mikoa wa Mbeya na Morogoro, tuna maeneo mazuri ya Mpunga, kwa nini Serikali isihamasishe watu wawekeze kwenye maeneo hayo?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kusema naunga mkono hoja, yangu mengine yote nitayaandika kwa maandishi. Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi asubuhi ya leo, naomba nianze na pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri na timu yao yote kwa kutuletea bajeti nzuri sana, sana, sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais amethubutu, leo tunazungumzia Tanzania ya viwanda kwa vitendo na mimi ndiyo Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Viwanda, nasema sera inatekelezeka! Wanaosema sera haitekelezeki, waje kwenye kamati yangu. Twende Kibaha tukaangalie viwanda vipya vilivyojengwa, twende maeneo yote tukaangalie viwanda vilivyoshamili, njooni tuangalie wawekezaji wanavoingia Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sera ya viwanda inatekelezeka kwa vitendo na Mheshimiwa Rais tumemshauri kama Kamati, akae na wadau azungumze nao, amekuwa msikivu, amekaa na wafanyabiashara, amekaa na wadau na amewasikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais, ni Rais wa mfano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanaozungumza maneno ya pembeni wameishiwa hoja, Mwenyekiti wa kamati ndiyo mimi. Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda ndiyo mimi, ukweli naujua mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amefanya mambo ambayo tumemshauri sisi, zile tozo zote zilikuwa ni kero, leo tozo 54 zimeondoka, siyo jambo dogo. Hilo ni jambo kubwa na la mfano na la kuigwa na la kupongezwa na ametekeleza Ilani ya chama chake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais katika hili tunakupongeza, tuko na wewe, kanyaga twende. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Bashungwa, nimpongeze Ndugu Mhede, karibuni katika mchakato huu tusaidiane tufanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongee kidogo muda unakwenda, nizungumzie suala la TRA. TRA kuna utaratibu ambao unasababisha wafanyabiashara na Watanzania wapate shida. Shida namba moja ni zile fomu za TIN, fomu zile zinaandikwa kwa kiingereza, wale wafanyabaishara wanapata shida kuzijaza, fomu zile zina urasimu, matokeo yake kuna vishoka wamekaa nje kwenye Ofisi za TRA, wanachukua zile fomu wanawajazia watu na vishoka wale wanawa-charge Watanzania shilingi 10,000 hadi shilingi 20,000; TRA tubadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, fomu zile zimepitwa na wakati, wakati fomu zile zinaandaliwa nchi ilikuwa haina Vitambulisho vya Taifa, sasa hivi tuna vitambulisho vya Taifa vina kila kitu ndani, anuani zote zimo ndani, kile kitambulisho kinatosha kabisa kutengeneza fomu ambayo ni very simple na fomu hizohizo zina matatizo upande wa BRELA, nawaomba TRA waliangalie hili, fomu zilizopo zinaleta urasimu na vishoka tunawapa muda wa kutafuta fedha nje ya utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka nilizungumze kwa upande wa TRA ni suala la kodi. Tumepunguza hizi kodi nyingi sana, sasa tunaomba wakasimamie ukadiriaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo lipo kwenye assessment, pale kwenye assessment ndiyo kuna matatizo, DG mpya tuna matumaini na wewe, ulikuwa Naibu Katibu Mkuu wa Viwanda nakufahamu uwezo wako. Nenda kaibadilishe TRA. TRA ikibadilika uchumi wa nchi utakua, TRA ikiwa rafiki wa wafanyabishara, tutasonga mbele kwa kasi kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee kidogo suala la fedha za kigeni, niongee na Gavana kama yupo. Hatua zinazochukuliwa na Serikali tunaziunga mkono, lakini naomba ifahamike, biashara za Dubai, China na nchi nyingine duniani, biashara kubwa hizi zimetawaliwa na suala la kulipa fedha taslimu. Unapokwenda Dubai kununua mzigo, ukinunua mzigo wa dola laki moja, wale wafanyabiashara wanataka cash dola laki moja. Sasa je, utaratibu wa kupeleka cash dola laki moja ukoje? BOT watusaidie namna bora ya kuhakikisha biashara zinarudi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kariakoo imepotea katika ramani ya biashara. Tulikuwa tuna Kariakoo ya Burundi, Rwanda, Malawi, Uganda na Congo, leo Kariakoo ile imepotea
kwenye mtandao haipo na sababu ya kupotea ile Kariakoo zipo nyingi ikiwemo suala la namna ya kupeleka fedha za kigeni Dubai, China na nchi nyingine, lakini leo kwa ruhusa yako Kamati ya Bajeti tulikwenda Uganda na mimi nilikwenda. Unafika Uganda unawauliza wafanyabiashara wa Uganda mbona siku hizi hamji Dar es Salaam kuchukua mzigo wanakwambia sasa hivi wa Dar es Salaam wanakuja kwetu, wa Malawi wanakuja kwetu, wa Rwanda wanakuja kwetu. Hayo ndiyo majibu tuliyopewa Uganda na wale bahari hawana, Bandari hawana. BOT tujiulize kuna nini hapo, TRA tujiulize kuna nini. Kwa nini tumelipoteza soko ambalo lilikuwepo Dar es Salaam, soko la Kariakoo. Bidhaa zile zilikuwa zinapatikana pale zina grade zake. Ukinunua mzigo kule Dubai, China kuna light weight, kuna heavy weight sasa zile biashara zilizokuwa zinafanyika TRA wao hawajui light, hawajui heavy, hawajui nini, wao ni kodi, kodi, kodi matokeo yake tumeua mtandao wa biashara, tumewakatisha tamaa wafanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunatakiwa tufungue milango ya Kariakoo, leo tunatakiwa tujiulize tumekosea wapi, tumekwama wapi. Mheshimiwa Dkt. Mpango tukae tusaidiane tufanye mawazo ya pamoja, tuzungumze hili tuna ushahidi, tuna nia ya kusaidia eneo hili lirudi katika mtandao wa biashara katika nchi zote za maziwa ambayo yametuzunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie Mfuko wa Mazingira; Kamati ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kulikuwa na Mfuko wa Mazingira ulikuwa una kazi nzuri ya kufanyakazi ya mazingira kwenye Nchi yetu. Mfuko huu mwaka jana 2018/2019 ulitengewa bajeti ya shilingi milioni 500 fedha zile hazikutoka. Dkt. Mpango alivyokuja kwenye Kamati ya Uongozi na Bajeti akaahidi 2019/2020 zile milioni 500 zitawekwa. Nashangaa, naona zile milioni 500 hazipo na ule mfuko hauna hata senti moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe ni mwanamazingira, Mfuko wa Mazingira hauna senti hata moja maana yake una zero na mfuko haupo. Nimuombe Dkt.Mpango rudisha kauli yako, zile milioni 500 ni ndogo mno tuanze na hizo. Tukipata shilingi milioni 500 tunaanza hapo. Hilo ni la Mfuko wa Mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba niende Mvomero; Mvomero tuna barabara ya lami inayoanzia Magole-Turiani- Mziha-Handeni-Korogwe. Barabara ile iliwekwa na Serikali makusudi ni barabara mbadala kwa ajili ya barabara ya Chalinze-Segera. Kilometa 48 zimeshawekwa lami Turiani- Magole bado Turiani-Mziha-Handeni. Mwaka huu niipongeze Serikali wameweka bilioni moja katika barabara hiyo, naomba sasa barabara hiyo itangazwe, mradi ule uanze ili barabara ile ifunguke. Wenzetu wa Handeni-Korogwe waliashaweka lami kwenye barabara yao.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee suala la mazao ya biashara; kule kwangu wanalima miwa, Kagera kule wanalima kahawa, Mwanza wanalima pamba, eneo hili tuna shida. Eneo hili tuna shida, nimpongeze Waziri amezungumzia kahawa na wanasema katika hotuba yake kwamba watalinda kahawa lakini mimi napata shida kidogo; hotuba ya kiingereza ya Waziri inazungumzia roasted coffee. Wale watu wa Kagera wanataka instant coffee inayokuja kutoka nchi za nje ndiyo ushuru wake upandishwe kwa sababu viwanda vilivyopo Tanzania vya instant coffee ndiyo vinapata ushindani mkubwa. Sasa kwenye hotuba yake amezungumzia kahawa, hotuba ya kiswahili amezungumzia kahawa, lakini kwenye hotuba ya kiingereza amezungumia roasted coffee.

SPIKA: Ahsante Mwenyekiti.

MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja mia kwa mia, ahsante sana. (Makofi)