Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Omary Tebweta Mgumba (1 total)

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali la kwanza.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, wewe ndiye Kiongozi wa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ndani ya Bunge, lakini pia ndiye kiranja mkuu wa Serikali hii ya Awamu ya Tano. Mheshimiwa Waziri Mkuu, kama unavyofahamu kuna wazabuni wengi katika Halmashauri zetu tunakotoka ambao sisi ni wawakilishi wao pamoja na Serikali Kuu, walifanya kazi ya kutoa huduma katika taasisi za Serikali na Serikali yenyewe kwa muda mrefu, wengine wana miaka miwili, mitatu, wengine mpaka mitano, lakini mpaka sasa hawajalipwa stahiki zao.

Mheshimiwa Waziri Mkuu ukizingatia mnamo tarehe 01 Juni ndani ya Bunge hili, uliliambia Bunge hili kwamba malipo yanachelewa ni kwa sababu wanafanya uhakiki, ambalo ni jambo zuri, kuwagundua wale ambao wanastahili kulipwa…

SPIKA: Swali Mheshimiwa Mgumba, moja kwa moja!

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu, watu hawa wamesubiri kwa muda mrefu na ukaguzi umeshafanyika zaidi ya mara tano, nini kauli ya Serikali, watawalipa lini wazabuni wote waliotoa huduma ndani ya Serikali?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mgumba, Mbunge wa Morogoro Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba, Serikali inadaiwa na wazabuni wetu waliokuwa wanatoa huduma kwenye maeneo mbalimbali. Wako ambao wametoa huduma kwenye Halmashauri za wilaya kwa maana ya huduma kwenye shule, kwenye magereza, lakini pia wako ambao wamefanya kazi za kutoa huduma kwenye Wizara mbalimbali. Na kwa mara ya mwisho nilikuwa hapa nilipata swali la aina hii linalowahusu wadai/wazabuni wa pembejeo, wote hawa ni watoa huduma ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumeweza kugundua kwamba baadhi ya madeni na baadhi ya wadai wachache miongoni mwao wametuletea taarifa za madai ambayo si sahihi sana. Na kweli, tulichokifanya tulitoa maagizo kwenye maeneo yote, ili kuhofu kupoteza fedha, kulipa fedha ambayo haikufanyiwa kazi kwa madai yale.

Kwa hiyo, tumeendesha zoezi la uhakiki chini ya Wizara ya Fedha na taasisi yetu kupitia CAG, hasa kule kwenye madeni makubwa ili kujiridhisha viwango vinavyotakiwa kulipwa kwa wazabuni hawa.

Mheshimiwa Spika, tuliweka utaratibu kwamba angalao kufikia mwishoni mwa mwezi huu tuwe tumemaliza hilo zoezi la uhakiki halafu tuanze kulipa madeni haya. Kwa hiyo ni matarajio yangu kwamba Wizara ya Fedha watanipa taarifa, na Wizara zile zote ambazo zina madeni ya watoa huduma zitatoa taarifa ya viwango vya fedha, halafu sasa tusimamie Wizara ya Fedha kuweza kuwalipa hawa watoa huduma.

Mheshimiwa Spika, nataka nitumie nafasi hii, kwanza niwashukuru kwa uvumilivu wao wadeni wote wanaotudai, lakini pili tuwasihi waendelee kutuvumilia na taratibu hizi kwa lengo lilelile nililokuwa nimelieleza awali la kuokoa fedha ambazo zinalipwa kwa watu ambao hawakutoa huduma. Hata hivyo bado tutaendelea kuwatumia watoa huduma kutoa huduma ndani ya Serikali kwenye maeneo ambayo wameendelea kutoa huduma na tuwahakikishie tu kwamba tutawalipa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge kama wako watoa huduma kwenye eneo lako endelea kuwahakikishia kwamba Serikali tutlipa madeni. Ahsante sana.