Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Japhet Ngailonga Hasunga (CPA) (68 total)

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa Mpango huu ambao ametuletea, Mpango wa Pili wa Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 mpaka 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli nimefurahishwa sana na Mpango huu ambao umeletwa mbele yetu. Mpango huu umeeleza bayana vipaumbele ambavyo Serikali inategemea kutekeleza katika kipindi hiki cha miaka mitano.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika vipaumbele hivyo ambavyo ni msingi mkubwa sana wa maendeleo ya nchi yetu mambo yako mengi lakini suala la kwanza ambalo ni la msingi sana ni kuendeleza kilimo. Suala la kilimo inabidi lipewe kipaumbele cha kutosha. Kilimo ndiyo uti wa mgongo wa maendeleo ya nchi yetu, kilimo ndiyo kinachotoa ajira kubwa kwa wananchi wengi katika nchi yetu, zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wanategemea kilimo. Pia tunapotaka kuipeleka nchi kuwa ya viwanda tunategemea zaidi kwamba malighafi nyingi na mazao mengi yatakuwa ni yale yanayotokana na kilimo na hivyo viwanda vingi ambavyo tunavianzisha vitakuwa vile vitakavyochakata mazao yanayotokana na kilimo. Naomba tuongeze jitihada kabisa za kuhakikisha tunakiimarisha hiki kilimo, pembejeo zile zinazohitajika katika kufufua kilimo hiki ziongezeke na bajeti ya kilimo iongezeke ili kwenda kujenga nchi ya uchumi safi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiofichika kwamba kama tukikifufua kilimo, tukiimarisha viwanda vinavyotokana na mazao ya kilimo, asilimia kubwa sana ya watu wetu wataajiriwa. Nashauri Serikali ihakikishe tunajenga viwanda vitakavyochakata mazao haya ya kilimo. Viwanda hivi vitasaidia sana kutoa ajira na msukumo mkubwa katika kuchangia pato la Taifa.
Kipaumbele cha pili ambacho kinaendana na hicho cha kilimo ni kuimarisha miundombinu mbalimbali ambayo ita-support hicho kilimo chetu. Miundombinu ya barabara, umeme na vitu vingine vinavyoendana na hivyo vitasaidia sana kuhakikisha nchi yetu inaendelea. Pia miundombinu hiyo itatoa ajira kwa vijana wetu wengi katika nchi yetu. Kwa hiyo, lazima tuweke nguvu zaidi katika kuimarisha hiyo miundombinu ya reli na vitu vinginevyo.
Nimefarijika sana na jitihada za Serikali za kuamua kufufua Shirika letu la Ndege. Katika ulimwengu huu kila nchi ina shirika lake na Shirika la Ndege ndiyo linatoa mchango mkubwa sana katika kuendeleza nchi. Tumeona nchi mbalimbali jinsi zinavyofanya. Kwa kweli inasikitisha sana kuona shirika letu limekuwa likisuasua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi jitihada ambazo Serikali ya Awamu ya Tano imeamua kuzichukua katika kulifufua shirika hili lazima tuziunge mkono kwa udi na uvumba ili kuhakikisha linakua na linatoa ajira nyingi kwa vijana wetu lakini pia tuweze kulitumia katika kuharakisha kuchochea maendeleo katika sehemu mbalimbali. Shirika letu sasa hivi lina ndege moja au mbili …
WABUNGE FULANI: Hamna.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri hizi ndege ambazo tumepanga kuzinunua zikinunuliwa naamini zitachochea sana maendeleo ya nchi yetu. Kwa hiyo, tuongeze hizo jitihada. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ili tuweze kuleta maendeleo ya kweli lazima huduma mbalimbali zikiwemo huduma za masuala ya fedha ziimarike. Hivi sasa mabenki mengi yamekuwa yakifanya biashara maeneo ya mijini hayakuweza kwenda vijijini. Sasa hivi Benki ya Wakulima imeanzishwa lakini bado iko Dar es Salaam. Nashauri kama ni Benki ya Wakulima ianzishwe mikoani ili wakulima wapate nafasi ya kwenda kukopa huko na tuweze kufufua kilimo chetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia mabenki yetu mengi yalikuwa yanafanya biashara kwa kutegemea fedha za Serikali. Kwa hiyo, naomba niunge mkono jitihada za Serikali, sasa hivi za kuhakikisha fedha zote za Serikali zinakuwa Benki Kuu ili mabenki haya yaende sasa kutafuta wateja huko vijijini na hii itasaidia sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo, wakati Serikali inachukua jitihada za kubana matumizi na hivyo kuondoa fedha nyingi za Serikali kwenye mabenki maana yake sasa mabenki nayo lazima yafanye jitihada za makusudi za kuhakikisha kwamba riba za mikopo zinashuka. Sasa hivi riba ziko juu sana, wananchi wakikopa baada ya miaka miwili, mitatu unakuta deni ni mara mbili ya kile ambacho alikuwa amechukua hali ambayo haisaidii kuchochea maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nadhani kwa kuangalia riba zile za kukopa na riba ambazo wanazitoa kuna spread kubwa ambayo nafikiri Serikali pamoja na mabenki yachukue hatua zinazostahili kuhakikisha kwamba yanarekebisha hiyo hali ili kusudi benki hizi zichochee maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mpango huu umejikita katika utoaji wa huduma za jamii hasa suala la elimu. Suala la elimu limepewa uzito mkubwa na naunga mkono kwani bila kuimarisha elimu hatuwezi kuwa nchi ya kipato cha kati. Elimu hii ndiyo itakayotuwezesha tupate watalaam wazuri, tupate watalaam wa kati wanaohitajika katika viwanda vyetu. Lazima mitaala ya elimu zetu kuanzia shule za msingi, sekondari, vyuo vya kati na vyuo vikuu ipitiwe upya ili iendane na mahitaji halisi ya wakati tulionao. Hilo naamini linawezekana kwa kutumia watalaam na uwezo uliopo tunaweza tukafanya kazi nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vyetu vinahitaji wataalam, sasa hivi vijana wengi wamekuwa wakikimbilia sana kwenda kusoma kwenye vyuo vya elimu ya juu wanakuwa ni ma-engineer, lakini nadhani kuna haja ya kuimarisha elimu ya mafundi wale wa kati na hasa vyuo vyetu hivi vya VETA na vyuo vinginevyo. Hivi ndivyo vitakavyoweza kuchukuwa vijana wengi na kuwapa ujuzi unaohitajika katika viwanda vingi. Kwa hiyo, hizi jitihada lazima ziungwe mkono kwa hali na mali ili tuhakikishe kwamba tunafika kule tunakokusudia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kupongeza Serikali ya Awamu ya Tano ya kuhakikisha kwamba elimu yetu inakuwa bure kwenye shule za msingi na sekondari mpaka kidato cha kumi na mbili. Kwa kweli hili ni suala zuri sana lazima tuipongeze Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tumeanza kuitekeleza hii sera imeonyesha matumaini na matunda makubwa kwani watoto wengi wameweza kwenda shule na kuandikishwa. Sasa lazima tuhakikishe kwamba tunaunga mkono jitihada hizi na tunashirikiana na Serikali ya Awamu ya Tano ili kuhakikisha hii azma inatekelezeka. Zipo changamoto ambazo tutakabiliana nazo na ni kitu cha kawaida. Unapoamua kuanzisha kitu chochote lazima ukabiliane na changamoto ambazo naamini tutashinda na tutafika mahali pazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuzungumzia suala la afya. Jitahada za Serikali ya CCM sasa hivi ambazo tumejikita nazo na tumeiweka kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi kwamba kila kijiji kuwe na zahanati na tunataka kila kata kuwe na kituo cha afya lakini vituo hivi vya afya vinahitaji pia viwe na wataalam. Jitihada ambazo wananchi wameanza kuonyesha kwa kujenga zahanati na vituo vya afya, Serikali iongeze mkakati wa kuhakikisha inawaunga mkono na pale ambapo wamekamilisha vianze kufanya kazi kama ambavyo inakusudiwa. Wananchi wamejitoa sana kuhakikisha wanajenga hivi vituo vya afya na zahanati, Serikali itekeleze wajibu wake pale ambapo tunaona kwamba panatakiwa kutekelezwa ili kusudi maendeleo yapatikane haraka kadri inavyowezekana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, Mpango huu ni mzuri, mpango wa kuimarisha reli ya kati, mpango wa kujenga reli kwa standard gauge ni wa muhimu sana kwani utatusaidia sana kuchochea maendeleo katika mikao yote. Hii ndiyo njia pekee itakayotusaidia nchi yetu kuweza kuunganishwa na hizo nchi zingine na kupunguza gharama za uendeshaji ambazo sasa hivi zimekuwa ni kubwa sana. Sasa hivi barabara zetu zinabeba malori makubwa ambayo yanasababisha barabara zetu zisidumu kwa muda mrefu. Kwa hiyo, tukiimarisha reli hii naamini itakuwa limesaidia sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na hayo machache, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JAPHET H. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipatia nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Ofisi ya Rais, Utumushi na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba niwapongeze sana Waheshimiwa Mawaziri wote wawili kwa kazi kubwa ambayo wameifanya na ambayo wameendelea kuifanya. Kwa kweli nawapongeza sana tena sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba kuchukua nafasi hii kuipongeza Serikali kwa ujumla, Serikali ya Awamu ya Tano ambayo imekuwa ikifanya kazi nzuri sana katika kuhakikisha kwamba maendeleo ya nchi hii yanasonga mbele. Kwa kweli hongera sana Serikali ya Awamu ya Tano.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kuchangia kwanza katika mapato ya halmashauri. Katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri ameeleza kwa undani sana hatua ambazo Serikali inakusudia kuchukua ili kuhakikisha kwamba inaimarisha mapato na mimi naunga mkono hizo jitihada ambazo Serikali inategemea kuchukua. Hata hivyo, kuna haja ya kuwa na mfumo mzuri kabisa, mfumo madhubuti wa kuhakikisha vyanzo vyote vya mapato vya Halmashauri vinasimamiwa vizuri. Bila kuwa na mfumo mzuri wa kusimamia mapato, tutapata matatizo makubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Serikali inasema tutaachana na mawakala ambao walikuwa wanakusanya Halmashauri zitaanza kukusanya zenyewe kwa kutumia mfumo wa electronic. Nashauri kwamba wakati tunakwenda kwenye huu mfumo basi ni vizuri Halmashauri zitakapowapangia wale watendaji wanaokwenda kukusanya wahakikishe kwamba wanawapa malengo na malengo hayo yasimamiwe vizuri ili wale watakaoshindwa kufikia malengo wachukuliwe hatua za dhati kabisa. Kwa sababu bila kufanya hivyo usimamizi wa mapato bado utaendelea kuwa mgumu na maeneo mengi kutakuwa na matatizo mengi sana ambayo tulikuwa tunayapata huko nyuma.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, nimeshukuru suala la property tax kwamba sasa itakuwa inakusanywa na Halmashauri. Mimi nataka niongezee tu kusema kwamba property tax ilikuwa haikusanywi vizuri na ni eneo ambalo lina mapato mengi. Ukiangalia nyumba ambazo zipo katika maeneo ya mijini na maeneo mengine ni nyingi sana lakini nyingi zimekuwa hazilipi property tax. Kwa hiyo, ni vyema Halmashauri ziweke utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba majengo na maeneo yote yanalipa hiyo property tax ambayo itasaidia kuinua vyanzo vya mapato vya Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo napenda nichangie ni kuhusu malipo ya walimu ambao walisimamia mitihani ya kidato cha nne mwaka jana. Walimu hawa walifanya kazi nzuri sana, walisimamia kwa uadilifu, walisimamia kwa uaminifu mkubwa na kazi yetu ikawa imekamilika vizuri. Kwenye Wilaya yangu ya Mbozi wale walimu mpaka leo hawajalipwa, naambiwa walilipwa posho ya siku tatu tu. Hili ni tatizo kubwa kwani linawavunja moyo sana walimu hawa ambao bado wana kazi kubwa sana ya kufanya na kuchangia katika maendeleo ya nchi hii. Juzi Mheshimiwa Waziri alitoa tamko kwamba sasa wanafanya jitihada kuhakikisha kwamba haya malipo yanakamilika. Naiomba Serikali itutamkie ni lini hasa ambapo walimu hawa watalipwa hayo malimbikizo yao ya hela zao za kusimamia mtihani, itatusaidia sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ambalo napenda kuchangia ni hili suala la fedha shilingi milioni 50 ambazo tumejiwekea kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambazo tutapeleka katika vijiji na vitongoji. Hizi fedha zikienda tutakuwa tumefanikiwa kwa kiwango kikubwa sana, zitatusaidia sana. Hata hivyo tuwe na mfumo mzuri wa kuhakikisha kwamba hizi fedha zitakapokuwa zinatolewa basi wale wanaokopa utaratibu wa kurudisha ieleweke ni wapi watakuwa wanarudisha na wengine watakuwa wanakopa na wengine wanarudisha. Kwa hiyo lazima, tuwe na mfumo ambao unaeleweka vizuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo napenda kuchangia ni kuhusu afya. Kule Mbozi katika Jimbo langu la Vwawa, wananchi wameitikia wito sana wa kujenga zahanati na kushiriki katika ujenzi wa vituo vya afya. Zahanati nyingi zimejengwa ziko zaidi ya 40 na zimekamilika toka mwaka jana mpaka sasa hivi bado hazijafunguliwa. Naomba Serikali ije na mkakati ituambie ni lini hasa hizo zahanati zitafunguliwa ili zianze kufanya kazi kusudi wananchi waendelee kupata huduma zinazostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia napenda kuchangia kuhusu mafunzo ya awali kwa watumishi wa umma. Mafunzo ya awali kwa watumishi wa umma ambao wanaajiriwa kwa mara ya kwanza ni muhimu sana. Hivi sasa tumekuwa tukishuhudia kumomonyoka kwa maadili katika maeneo mengi. Watumishi wa umma wanapoajiriwa wakitoka mitaani wanakuwa bado hawajui miiko na utamaduni wa kufanya kazi kwenye utumishi wa umma. Sheria hii imeweka ni lazima ndani ya miezi sita wanatakiwa wapate mafunzo lakini hivi sasa waajiri wengi wamekuwa hawatekelezi agizo hilo. Naishauri Serikali ni vyema kuhakikisha kwamba ndani ya kipindi kile cha miezi sita wale watu wanapokuwa wameajiriwa kwenye utumishi wa umma wapatiwe mafunzo ili waweze kujua ni namna gani wanatakiwa kuendesha kazi zao na namna gani Serikali inatenda kazi zake. Hiyo itatusaidia sana katika kupunguza matatizo ambayo yamekuwa yaliyopo katika utumishi wa umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo la mafunzo ya awali lakini pia mafunzo elekezi. Mafunzo elekezi ni muhimu sana kwa watumishi wa umma hasa wale ambao wanakuwa wamefikia katika ngazi za kati na wanajiandaa kwenda kwenye ngazi za juu. Bila kupata mafunzo ya uongozi, mafunzo ya menejimenti hawa watu wanakuwa ni vigumu sana kuelewa. Kuna wengine wanakuwa ni wataalam wa fani zingine lakini unapokuwa umepata madaraka ya uongozi unatakiwa uongoze watu, kwa hiyo, ni lazima ujue masuala ya uongozi yanasemaje. Maana unatakiwa usimamie fedha, usimamie mali mbalimbali sasa lazima upate mafunzo ya kutosha kuhakikisha wanatenda kazi zao inavyotakiwa. Kwa kweli nashauri wote wapatiwe mafunzo haya elekezi hiyo itasaidia sana.
MHE. JAPHET H. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza jina langu naitwa Japhet Hasunga, siyo Joseph.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kwanza kushukuru kwa kupata nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii. Pia napenda nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa hotuba nzuri ambayo ameitoa na mchanganuo mzuri ambao ameuwasilisha leo hii, kwa kweli nimefurahi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuipongeza Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa uchambuzi wa kina walioufanya na kuiwasilisha katika Bunge lako Tukufu. Kwa kweli ni nzuri sana na imejenga msingi mzuri wa nini kinatakiwa kufanyika katika Wizara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuchangia katika Sera ya Elimu ya shule za msingi na sekondari ya mwaka 2014. Sera hii ni nzuri sana ambayo imeandaliwa na iliwasilishwa na ilishirikisha wadau mbalimbali ambayo imeweka bayana hatua ambazo zinatakiwa kuchukuliwa na Serikali kuhakikisha kwamba nchi yetu inabadilika kwa hali tuliyonayo na kwenda mahali ambapo ni pazuri. Elimu ni kitu muhimu sana, elimu ndiyo msingi mkubwa wa maendeleo ya nchi yoyote na hii ndiyo itakayotusaidia kutufikisha kuwa nchi ya kipato cha kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika elimu hii sasa hivi vijana wetu wengi ambao wamekuwa wanamaliza elimu ya msingi, wanamaliza wakiwa ni wadogo sana, wengi wanaanza darasa la kwanza wakiwa na miaka mitano, miaka sita wanamaliza shule ya msingi wakiwa na miaka kumi na mbili, kumi na tatu. Hivyo hawa-qualify kujitegemea wala hawawezi kujiajiri wala kuajiriwa, kwa sababu itakuwa ni kinyume na sheria za ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hilo sera hii ilikuwa inasema elimu ya msingi sasa itajumuishwa na elimu ya sekondari mpaka kidato cha nne. Mtoto akianza shule ya awali aende moja kwa moja shule ya msingi, akimaliza shule ya msingi anaunganisha moja kwa moja kwenda kidato cha kwanza. Kwa hiyo, ina maana watoto wote sasa watakuwa wanakwenda mpaka kidato cha kwanza wanamaliza mpaka kidato cha nne. Hapa mpaka wanamaliza sasa watakuwa wamefikisha umri ule ambao kidogo wanaweza wakaanza kujitegemea au wakaajirika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili nafikiri ni la msingi sana. Sasa nataka Wizara wakati wa majumuisho itupe maelezo ni hatua gani au mikakati gani wameiweka kuhakikisha kwamba sera hii sasa inaanza kutekelezwa kama ambavyo tulikusudia. Kwa sababu ifikapo mwaka 2018 ni kesho kutwa tu tutakuwa tumefika. Tungependa kikifika kipindi hicho watoto wote sasa wawe na uwezo wa kufika hadi kidato cha nne, badala ya kuishia darasa la saba ambapo wanakuwa kidogo hawajaandaliwa vya kutosha hilo ni la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna suala la watoto wanaopata mimba wakiwa shuleni. Mimba inapatikana kwa bahati mbaya, nasema ni kwa bahati mbaya siyo kwa makusudi, watoto wengi wamekuwa wakipata mimba kwa bahati mbaya mashuleni. Sasa watoto hawa wanapopata mimba, ni bahati mbaya unakuta kwamba baada ya muda wanaondolewa mashuleni kwa sababu eti wana mimba. Hii inakuwa ni kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pia ni kinyume na dira ya Wizara ya Elimu ambayo imeitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ninukuu, ukurasa wa nne pale, ameeleza dira vizuri sana, kwamba dira ya Wizara ni kuwa na Mtanzania aliyeelimika na mwenye maarifa, stadi, umahiri, uwezo na mitazamo chanya ili kuweza kuchangia katika kuleta maendeleo ya Taifa. Hivi ndivyo dira inavyosema na hii dira haijabagua mtoto wa kike wala kiume. Kwa hiyo ina maana watoto wote ni muhimu na mtoto wa kike sasa hivi ndiyo muhimu sana kumwelimisha kuliko hata mtoto wa kiume. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda kabisa kwamba hawa watoto ambao kwa bahati mbaya wanapata mimba basi wapewe nafasi ya kuendelea kusoma pale wanapokuwa wamejifungua ili kusudi waendelee kuelimika maana nao ni Watanzania kama Watanzania wengine. Hili ni la msingi sana na litatusaidia kuhakikisha kwamba sasa jamii yote ya Kitanzania Watanzania wote wanapata elimu sawa na ile ambayo tulikuwa tunakusudia. Nadhani kwamba hilo ni suala la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa nichangie katika hii Wizara ni kuhusu Mitaala. Mitaala ya elimu yetu kuanzia shule za msingi, sekondari, vyuo vya kati na vyuo vikuu lazima hii mitaala iangaliwe kwa undani ili iendane na maarifa na stadi zinazohitajika sokoni. Iwaandae vijana wetu kujitegemea, iandae wataalam watakaochangia na watakaoweza kushiriki katika maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa mitaala yetu haijaainisha vipaumbele ambavyo Taifa kama Taifa linahitaji. Watu wanasoma tu wengine wanajiunga katika vyuo mbalimbali, sasa vyuo hivi viendane na mahitaji halisi ya soko, ndiyo itatusaidia sana kwenda na wakati. Hili ni la muhimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa nilichangie ni kuhusu tafiti yaani research na project mbalimbali ambazo vyuo mbalimbali vimekuwa vikiwapa vijana wanafanya katika maeneo mbalimbali. Sasa hivi vyuo vingi havijatilia mkazo sana katika upande wa utafiti, vyuo vikuu vingi havifanyi utafiti wa kutosha. Bila kufanya utafiti wa kutosha hatuwezi kupata wataalam, hatuwezi kupata maendeleo halisi. Lazima vifanye utafiti na Serikali itenge fedha za kutosha kwa ajili ya kuhakikisha hao wataalam wetu wanafanya utafiti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti hizi ndizo zinatakazosaidia kuboresha mazingira na kuleta maendeleo katika nchi yetu. Kuna maeneo mengi ambayo vijana huwa wanafanya na kuna baadhi ya project ambazo vijana huwa wanapewa wakiwa mashuleni. Wanafanya project nzuri sana. Naishauri Wizara iandae utaratibu mzuri wa kuhakikisha zile project ambazo vijana wanafanya wakiwa vyuoni zingine zinafaa sana kuendelezwa, zingine zingefaa sana katika kuanzisha viwanda vidogo na kadhalika. Wanafanya ubunifu mzuri sana ambao nafikiri ni muhimu sana kama Wizara itakuwa na utaratibu mzuri, wa kuziangalia hizo project na kuangalia namna ambavyo Serikali inaweza ikazi-fund ili ziweze kuchangia maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa nichangie ni kuhusu Vyuo vya Ufundi, Vyuo vya VETA, pamoja na Vyuo Vikuu, Jimbo langu ni Makao Makuu ya Mkoa mpya wa Songwe na hiyo naipongeza Serikali sana. Pamoja na kuwa ni Makao Makuu ya Mkoa sasa hivi hatuna chuo hata kimoja, hatuna chuo cha Serikali wala cha watu binafsi. Sasa ni wakati muafaka naomba Wizara yako iangalie utaratibu, iweke utaratibu wa kuhakikisha kwamba Jimbo la Vwawa hasa Wilaya ya Mbozi tuna jenga chuo cha VETA ambacho kitawaajiri vijana mbalimbali waliopo katika Wilaya ile. Wale vijana wako maeneo mengi, iwe ni katika fani mbalimbali wapate ule ujuzi ambao utasaidia sana katika kuchangia maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Vyuo vya Elimu ya Juu kikiwemo Chuo Kikuu Huria, tungeomba vianzishe matawi haraka ili wananchi wale ambao ni wengi sana katika ile Wilaya waweze kupata elimu ile ambayo inahitajika katika hili eneo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa nichangie ni kuhusu suala la hii SDL, hii kodi ambayo sekondari za watu binafsi na vyuo vya watu binafsi vinatakiwa kulipia, SDL ya five percent. Kwanza naomba ku-declare interest kwamba mimi ni mdau na nina maslahi katika hili, hili suala sasa hivi sekondari zote za watu binafsi pamoja na vyuo binafsi vinaendelea kudaiwa SDL kwamba lazima vilipwe, wakati navyo vinatoa mafunzo ya ufundi ambao vinawaandaa vijana wale wale na sera za nchi hizi zinasema elimu siyo sehemu ya biashara, elimu ni kutoa huduma. Sasa kama ni huduma kwa nini vidaiwe SDL badala ya kupata mgao kutoka Serikalini unaotokana na hizi fedha, wanaambiwa wao wachangie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili kwa kweli halikubaliki kabisa, ningeomba kabisa kabisa kwa dhati Serikali iliangalie upya ili hizi shule za watu binafsi, vyuo vya watu binafsi, vipewe msaada, vipewe mgawo wa hii SDL ili viweze kujenga ujuzi, stadi na maarifa mbalimbali yanayohitajika katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri haya masuala ya msingi sana na naamini tukiweka misingi mizuri ya kuimarisha elimu yetu nchi yetu itapiga hatua sana. Wale wanaobeza kwamba nchi yetu elimu yetu inashuka, hapana haishuki tuendelee kuiboresha, tuweke mikakati mizuri, tuiimarishe, naamini nchi yetu itapiga hatua sana. Wenzangu wale ambao wanategemea kwamba eti mwaka 2020 tutaishia hapa labda CCM itaporomoka, nataka niwaambie CCM mwaka 2020 tutashinda huenda Viti vyote vya Ubunge kwa sababu ya kazi nzuri ambayo tutaifanya. Hii Wizara naomba ifanye kazi nzuri na mambo yatakwenda vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru sana kwa kunipatia hii nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza Mawaziri wote waliowasilisha bajeti zao na kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya, kwa kweli hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kila sababu ya kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano na hiyo ndiyo kazi yetu kubwa na sababu kubwa ambazo zinafanya tuipongeze ni mambo makubwa ambayo imefanya katika kipindi cha mwaka mmoja na nusu; katika mwaka mmoja na nusu huu mambo makubwa yameonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona kabisa jinsi nchi hii ambavyo sasa tunaibadilisha, kwa kweli hii tunajivunia sana. Lakini hii imeonesha dhahiri namna ya kupambana na rushwa katika nchi hii ambayo ilikuwa ni kikwzo kikubwa sana katika maendeleo yetu ya nchi, kwa kweli hii tunaipongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia imeonesha namna ya kupambana na dawa za kulevya, ni lazima tuziunge jitihada hizi kwa hali na mali ili kuhakikisha kwamba tunairekebisha nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo naomba nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwanza kwa kuanzisha rasmi mkoa wa Songwe, tunawashukuru sana tena sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naomba niipongeze Serikali katika mambo ambayo yalishindikana miaka mingi yameweza kutekelezeka, suala la elimu bure, lakini suala kubwa zaidi na ambalo hatutalisahau kwenye historia, ni suala la kuhamia Dodoma. Serikali yote imehamia Dodoma. Tumeimba miaka mingi sana, lakini sasa Serikali hii imeonyesha dhahiri kwa vitendo ndani ya mwaka mmoja na nusu Serikali karibu yote imehamia Dodoma na mimi naamini na ninamshauri Mheshimiwa Rais ahamie na yeye mapema kabisa kuliko ile ratiba tuliyoitoa. Kwa kweli tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali imefanya mambo mengine makubwa, tumeona kabisa tumeanza kujenga reli kubwa ya kati (standard gauge), reli ambayo tulikuwa tunaimba tu kwa muda mrefu. Hii itachangia katika kuongeza na kupanua uchumi wetu. Kubwa zaidi tumeweza kununua ndege ambazo hazikuwepo. Sasa tunalifufua Shirika letu la Ndege, haya ni mambo makubwa ambayo yamefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali. Kwa Jiji la Dar es salaam tumeona, tulikuwa hatujawahi kuona flyover Dar es Salaam; sasa flyover zinaanza kujengwa. Sasa tunataka nini zaidi? Ni mwaka mmoja tu na nusu yote haya yameonekana. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali kwa yote haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie masuala ya utawala bora. Masuala ya utawala bora nashangaa! Tusiyaangalie katika upana mdogo, tuyaangalie masuala ya utawala bora katika uwanja mpana sana. Masuala ya utawala bora yana mambo mengi. Kwanza kuna misingi ambayo tunaita ni misingi ya utawala bora, misingi ambayo ipo na misingi hii imewekwa kwenye Katiba, imewekwa kwenye mihimili yetu mitatu. Utawala bora ni jinsi ninyi mnavyoliongoza Bunge, mnavyozingatia kanuni, sheria, yote hayo ni utawala bora. Jinsi Wabunge tunavyochangia hapa ndani na watu wanavyochangia mawazo, ni utawala bora, jinsi Mahakama zinavyofanyakazi, ni utawala bora na jinsi Serikali inavyotenda kazi ni utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna Serikali duniani inayoweza ikafanya 100 percent, upo upungufu mdogo mdogo, lakini mambo ya msingi yanakwenda lazima tuyafurahie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utawala bora una mambo karibu kama nane hivi ambazo tunaita pillars za good governance. Kuna uwazi, uwajibikaji, demokrasia, ushirikishwaji, Serikali sikivu, kuna utawala wa sheria, kuna ufanisi na tija na kuna haki na wajibu. Haya yote yanasimamiwa vizuri na Serikali yetu. Sasa wapi kuna tatizo? (Makofi)
Mambo yanakwenda!
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia sasa hivi uwajibikaji ndani ya Serikali ni mkubwa, ukiangalia tunavyopambana sasa na kuondoa wale wote wenye vyeti hewa ni mapambano mazuri, ni uwajibikaji, ni utawala bora, tunapojenga nidhamu ya utumishi ni utawala bora. Sasa tunataka nini zaidi ili tuseme utawala bora upo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mengine tunayoyasema, dosari ndogo ndogo zipo. Hata mtawala Lee Kuan Yew, Baba wa Taifa wa Singapore, alisema hakuna mtu anayeweza akawa 100 percent perfect na hakuna njia sahihi duniani. Sisi tumeamua kuendeleza nchi, tutaendeleza, tutakwama, tutarudi nyuma, lakini tutasonga mbele, maadamu dhamira yetu iko pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tushirikiane, tuiunge mkono Serikali yetu jinsi ambavyo imekuwa ikitekeleza majukumu yake. Yapo masuala machache labda niseme madogo yanayohusu wachache wanaokwamisha utawala bora.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sasa hivi labda niseme, kule Jimboni kwangu Vwawa, hivi tunavyoongea leo tunachangia Wizara ya TAMISEMI. Eti nao Mwenyekiti ameitisha vikao vya Madiwani kule leo, nao wanaendelea eti wanaitisha vikao. Sasa Serikali ilishaelekeza, vikao vya Madiwani vitenganishwe na vikao vya Bunge. Mtaitishaje vikao hivyo? Kwa nini hayo yanafanyika? Yanafanyika kwa sababu ya maovu machache ambayo wanayafanya wengine, wanataka Waheshimiwa Wabunge tusishiriki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Jimboni kwangu kuna matatizo mengine makubwa na hapo naomba Serikali ichukue hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tume ziliundwa kuchunguza upotevu wa fedha zaidi ya mwaka mmoja hazijatoa majibu. Hiyo inakuwa ni dosari, hebu rekebisheni hayo. Pale kwetu kuna shilingi milioni 450 zimeenda kwenye miradi, watu wakagawana. Kuna shilingi milioni 680 za mradi wa maji Harungu, watu waligawana wakafanya uongo uongo, maji hayapo. Kuna shilingi milioni 320 za maji ya Ihanda, maji hayapo, wananchi wanahitaji maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ubadhirifu mwingi! Shilingi bilioni 1.8 yamefanyika Mbozi, hebu tupieni jicho angalieni Wilaya ya Mbozi, angalieni yanayoendelea mchukue hatua ili wananchi waendelee kuipenda Serikali yetu na wakipende Chama cha Mapinduzi na mimi naamini haya yanawezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wizara hizi naomba sana mtusaidie, kule tunahitaji maji. Kuna vijiji kama kijiji cha Iyula, Kijiji cha Iyula B, Vijiji vya Idiwiri, Igale, Nanyara, Senjere, vinahitaji maji. Huu mradi ulifanyiwa upembuzi yakinifu kwa muda mrefu haujatekelezwa. Tunaomba tusaidieni ili tuweze kuinua mazao mbalimbali likiwemo zao la kahawa tunaombeni sana hilo mtupe ushirikiano. Pia kuna mradi mwingine wa kutoka vijiji vya Lukururu, Mlangali, Mlowo ambao ungesaidia kuimarisha maji katika vijiji kama 14. Naombeni sana hilo mtusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Mji wa Vwawa pale pana shida ya maji, Makao Makuu ya Mkoa, hebu tusaidieni haya yaishe. Naomba pia sasa hivi kwa kuwa mmetupa Mkoa, naamini Mheshimiwa Waziri unanisikiliza vizuri kwamba umetupa Mkoa na nimewashukuru, sasa mtatupa na Manispaa ya Mkoa wa Songwe ambayo itakuwa Manispaa sijui ya Jimbo la Vwawa au ya Mbozi, yoyote ile. Tunaiombeni hiyo haraka ili tutekeleze majukumu yetu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaomba kwenye ule Mkoa barabara za mkoa; barabara ambayo itaunganisha Wilaya ya Mbozi na Wilaya yetu mpya ya Songwe. Tunaomba ile barabara mtupe, mtusaidie ili tuweze kuitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda suala la afya, kwenye Wilaya ya Mbozi wananchi wamejitahidi sana, wamejenga maboma, wamejenga zahanati, wamekamilisha wanahitaji wafanyakazi, wanahitaji dawa, hayo hayafanyika mpaka sasa hivi. Hebu tuungeni mkono, jitahidini kutuletea watumishi wa afya ili angalau tuweze kukamilisha na wananchi wawe na imani kwamba sasa mambo yanakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambalo ningependa nilizungumzie ni suala la ripoti ya Mkaguzi wa Nje (CAG). Nimeshangaa watu wengi wanaongelea sana hii CAG report. CAG report naomba Kamati maalum za kufuatilia…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na nashukuru sana kwa nafasi hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia kidogo kwenye Wizara hii ambayo ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi.

Kwanza napenda nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri ambayo ameitoa na mambo ambayo wanayafanya katika hii Wizara, kwa kweli nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli mchango unaotolewa na sekta hii ni mchango ambao hautoshelezi, haulingani na vivutio tulivyonavyo katika nchi hii. Nchi yetu ni nchi pekee duniani na nchi ya pili kwa kuwa na vivutio vya utalii duniani baada ya Brazil, ni nchi ambayo ina mlima mrefu katika Afrika na mlima wa pili duniani hicho ni kivutio kizuri sana. Ni nchi ambayo kwa mujibu wa wanasayansi mwanadamu wa kwanza duniani inasadikika aliishi hapa, hicho kivutio peke yake ni kikubwa sana katika nchi hii, wanasayansi wamegundua hilo, wameliona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ni nchi yenye mbuga nyingi sana za wanyama, ni nchi ina maziwa marefu, tuna maziwa mengi, tuna bahari tuna ziwa lenye kina kirefu duniani Ziwa Tanganyika, ni nchi ambayo kule kwenye Jimbo langu la Mbozi kuna kimondo ambacho ni cha aina yake hakipo duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni nchi ambayo watalii wanakuja kuangalia nyayo za watu waliopita miaka mingi walipo kanyanga tunapata hela nyingi sana. Ni nchi ambayo tumebahatika ambayo Mwenyezi Mungu kweli ametupatia kila kitu, lakini ukiangalia mchango wake kwenye Pato la Taifa haulingani na haya yote tulionayo, mikakati tuliyonayo hailingani na hali halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali sasa hivi kweli tumeanza kuchukua hatua za kuimarisha utalii, kwa mfano kwa sababu tumenunua ndege sasa za kusaidia kuimarisha utalii, hiyo peke yake haitoshi, yapo mambo mengi yanayotakiwa kufanyika ili kufufua utalii wetu. Kwanza lazima tuangalie kodi mbalimbali, tozo mbalimbali zinazotozwa kwenye sekta ya utalii, concession fees lazima ziangaliwe, ukilinganisha na wenzetu, ukilinganisha na Kenya, ukilinganisha na nchi zingine lazima tuangalie ni namna gani hizi kodi zinakuwa ni vivutio kwa watalii badala ya kuwa discourage, bila kufanya hivyo nchi hatuwezi kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya kitu cha muhimu sana katika sekta ya utalii ni kuimarisha miundombinu ya utalii, miundombinu hiyo ni pamoja na kujenga viwanja vya ndege kwenye maeneo mengi ambayo hiyo nadhani Serikali imeanza kufanya, tumenunua ndege, lakini hiyo haitoshi, tunahitaji barabara nzuri zinazoelekea kwenye vivutio mbalimbali, barabara zinazopitika ili watalii waweze kupita, lazima hayo yote yafanyike kwenda kule kwenye Jimbo langu kule kwenye kimondo barabara ni mbaya, tunahitaji hoteli za maana kwenye maeneo yale. Kule kwenye kimondo hakuna hoteli, hakuna barabara, hakuna nini, ni mtalii gani atakwenda? Sasa haya yote lazima tuyafanye ili kuhakikisha kwamba tunaimarisha sekta hii ya utalii ili iweze kutoa mchango mzuri na unaokubalika katika nchi. (Makofi)

Jambo la pili, hatujafanya jitihada za kutosha za kutangaza utalii. Ukiangalia matangazo yetu mengi ambayo tunayafanya hayatoshelezi, ukiangalia bajeti yetu tunayotumia kuitangaza bado ni ndogo, vivutio viko vingi lakini hatujavitangaza kama inavyotakiwa, bila kufanya hivyo hatuwezi kufika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tulikuwa tunachangia hapa tukawa tunasema angalia tulikuwa na Serengeti Boys, vijana wetu wameenda kule wanatutangaza, lakini hebu angalia mashindano mengi yamefanyika kwenye nchi hii, kuna Olympic huwa tunakwenda, kuna mashindano ya Jumuiya ya Madola huwa tunakwenda, kuna Kilimanjaro pale huwa tunakwenda yale mashindano yalikuwa na watu wengi sana, mwaka jana nafikiri walikuwa watu 11,000 walishiriki kwenye yale mashindano, Mount Kilimanjaro Marathon walishiriki, lakini angalia jezi ambazo wanavaa watu wetu, angalia jezi wanazokuwa wamevaa hazitangazi utalii, makampuni yetu yapo wapi kutangaza huo utalii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kuna wachezaji, kuna mmoja ameenda kule ameshiriki Uingereza ameshinda, lakini alikuwa na jezi anatangaza bia, jezi yake ile inatangaza Multi Choice ya South Africa na ametoka Tanzania, hiyo lazima tusikitike, lazima tuhakikishe tunakuwa very strategic tufanye maamuzi ambayo kweli yataisaidia katika kuimarisha nchi hii (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna michezo mingi inafanyika sasa hivi, najua tunajiandaa kwenda Japan, wenzetu Wakenya wanapoenda kwenye michezo kama hiyo huwa wanaomba mpaka space wanakuwa na space kule ya kutangaza, Ethiopia wanakuwa na space ya kutangaza wanakuwa na banda wanatangaza vituo vyao vya utalii pamoja na michezo, Watanzania tunagawa business card kwenye mabanda yetu, hatuna hata maeneo ya kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kuimarisha ili kuhakikisha kwamba kwa kweli mambo yaende vizuri, bila kufanya hivyo tutashindwa. Sekta hii ina mchango mkubwa sana ambao ninaamini kabisa unaweza kuchangia sana katika maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuangalie Ngorongoro, Serengeti na makampuni mengine yajaribu kudhamini michezo mbalimbali, tuna michezo mingi sana Tanzania, ikidhaminiwa tukawapa vifaa vizuri vya michezo kwa ajili ya kutangaza utalii, ninaamini tutajitahidi sana na tutaweza kufufua na kuisukuma mbele sekta yetu hii ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika mbuga zetu huku watalii wanapokwenda, zile huduma za msingi zinakuwa bado ni kidogo sana. Nimeangalia juzi walikuwa wanalalamika wanapopanda Mlima wa Kilimanjaro, wanapopanda wanasema kuna watalii wengine wanashindwa, wakishindwa kule hakuna hata helicopter ya kuwapa msaada, hakuna nini, hiyo inatuaharibia. Vifaa vya dharura vya kuweza kuwasaidia watalii wetu wanapokuwa wamepata dharura tuviimarishe katika maeneo yetu ili tuweze kusaidia katika hii sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia vyuo vya utalii nimeangalia hapa na mambo mengine mengi, ushiriki wa sekta binafsi yote ni mambo ya msingi sana, suala la msingi zaidi ili kuweza kuvutia watalii ni ulinzi na usalama ndani ya nchi yetu, bila kuwepo na usalama wa kutosha watalii wanaogopa hawawezi kuja.

Naiomba Serikali iweke utaratibu mahsusi, iweke mikakati ya kutosha kuhakikisha kwamba tunaimarisha ulinzi na usalama katika maeneo ya vivutio vyetu vya utalii na hiyo itasaidia sana kuweza kuleta mchango mkubwa na kuimarisha sekta yetu hii ya utalii ili iweze kutoa mchango mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mambo ya msingi sana katika hii Wizara na ni Wizara ambayo inaweza ikatubeba, tukichanganya hii na ya Madini kama leo tumesikia taarifa zingine za madini tukichanganya zinaweza kusukuma maendeleo kwa kiwango kikubwa sana katika nchi yetu. Kwa hiyo, lazima mikakati ya kutosha kabisa iwekwe hapo ili kuhakikisha hii sekta inaimarika.

Suala la pili ambalo ningependa kuchangia katika hii Wizara ni suala la misitu na utunzaji wa misifu. Hifadhi ya misitu iko maeneo mengi, kule Jimboni kwetu sasa hivi imekuwa ni kero kubwa sana katika utunzaji wa misitu, ile misitu miaka ya nyuma tulikuwa na machifu walikuwa wanalinda sana ile hifadhi, wananchi walikuwa hawakati kati ovyo, sasa hivi Serikali ikaja kuanza kushughulikia inawakamata watu ovyo hadi misitu ile imeanza kuharibika. Ninaamini kabisa kama tukiwatumia na tukiwashirikisha wananchi katika kulinda ile misitu inaweza ikalindwa vizuri kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ambalo limejitokeza sana kule Jimboni hii Wizara inatoa vibali kwa wakata mkaa, baadhi wanakata magogo, wanakata mkaa, wanauza lakini wananchi wakikutwa na mkaa wananyang’anywa na wanapigwa, wakati tayari hao wamepewa vibali, najua kuna wengine ambao wanakuwa hawana vibali lakini wapo wengine wana vibali, sasa inakuwaje wananchi wale wanaotumia mkaa wakati hawajaambiwa nishati mbadala hasa wanatumia mkaa wanakamatwa na bahati mbaya wanapokamatwa, wanaponyang’anywa ule mkaa haupelekwi Serikali. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JAPHET N. HASUNGA Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ili nami niweze kutoa mchango wangu katika bajeti hii ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kabisa kwa kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa bajeti nzuri ambayo ameileta Bungeni, tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii bajeti kwa kweli inatekelezeka, ina vipaumbele ambavyo vinakuna maisha ya kawaida ya Watanzania na ina mambo mazuri. Kwa hiyo, nadhani kazi yetu sisi kama Wabunge ni kuendelea kushauri labda marekebisho au nyongeza, mambo gani yaongezewe katika hii bajeti ili iweze kuwa nzuri zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianzie kwenye Sekta ya Kilimo. Kwenye Sekta ya Kilimo inaonekana kwamba kilikua kwa asilimia 1.7 kutoka asilimia 2.1. Sekta ya Kilimo ndio uti wa mgongo wa maendeleo ya nchi hii. Kuna sekta ambazo tukiweka nguvu ya kutosha tunaweza tukaleta maendeleo ya kweli katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, labda nitaje sekta chache. Tukiweka nguvu kwenye Sekta ya Kilimo, Ufugaji na Uvuvi, tukafanya vizuri, tunaweza kutoa mchango mkubwa sana katika nchi hii. Sekta hii ndiyo inayotoa ajira ya Watanzania walio wengi. Zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania wanategemea kilimo. Kwa hiyo, lazima tuiangalie. Sekta ya Nishati na Madini, tumeona madini yako mengi. Tukiimarisha hii, tukaweka vipaumbele vizuri, tukaifanyia vizuri, tutakuwa hatuna shida ya fedha za kuendesha nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, katika Sekta ya Maliasili, ukiangalia mbuga za wanyama tulizonazo, ukiangalia mlima mrefu katika Afrika na wa pili duniani, ukiangalia mambo mbalimbali yanayohusiana na utalii, tukiyawekea mkazo mzuri, tunaweza tukafanya kazi nzuri na maendeleo ya nchi hii yatakimbia haraka sana.

Mheshimiwa Spika, nirudi sasa kwenye Sekta ya Kilimo. Kwenye kilimo Serikali imesema, sasa hivi kwenye upande wa pembejeo wamesema tutafanya bulk procurement. Ni imani yangu kabisa kwamba Serikali itatekeleza mwaka huu vizuri kabisa. Tukifanya hivyo, pembejeo zitashuka bei na kuwawezesha wakulima wetu kuweza kupata pembejeo kwa bei nzuri na hivyo kuongeza tija na kuongeza uzalishaji wa mazao mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kule kwetu kwenye Jimbo langu la Vwawa, Wilaya ya Mbozi, sisi ni wakulima sana, lakini tunahitaji pembejeo zije kwa wakati na kwa bei nzuri. Hiyo itatusaidia sana kuchangia mchango mkubwa katika Taifa hili. Pia kuna zao la kahawa ambalo lilikuwa linaongoza Tanzania kwa kutuingizia fedha za kigeni. Zao hili sasa limeshuka, sijui sasa limeshika nafasi ya sita! Lazima Serikali tukae chini tuangalie nini kimetokea kwenye zao la kahawa ili tuweze kulifufua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona kabisa sasa hivi mazao kama korosho yameanza kuongezeka na yameongeza mchango mkubwa, lakini zao la kahawa, nini kimetokea? Hebu Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anajibu aangalie nini tufanye katika hilo?

Mheshimiwa Spika, kwenye ufugaji tuondokane na uchungaji, twende kwenye ufugaji wa kisasa. Sasa hivi hakuna ufugaji wa kisasa, kuna uchungaji katika nchi yetu. Tukifanya hivyo, tukiwa na mashamba ya ufugaji, naamini kabisa tutaona mchango wetu.

Mheshimiwa Spika, kuna bahari kuu kule, kuna deep sea, hatujaweka jitihada za kutosha kwenda kuvua. Wananchi wetu wanakufa, watoto wetu wanakufa kwa magonjwa mbalimbali yanayotokana na ukosefu wa chakula. Tungekuwa tumeimarisha uvuvi tukapata samaki, tukawalisha wananchi wetu, mimi naamini hata magonjwa yangepungua. Kwa hiyo, nadhani jitihada lazima zichukuliwe na Serikali katika kuimarisha hii Wizara ili tuhakikishe kwamba inatoa mchango mzuri katika kuimarisha uchumi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili katika upande wa kilimo, nimeangalia sana hii bajeti, inazungumzia subsistance agriculture. Hatuwezi kuendeleza nchi kwa kilimo kidogo kidogo hiki, lazima kama nchi twende kwenye commercial farming. Bila kwenda kwenye commercial farming hatutafika. Lazima jitihada ziwekwe. Nimeangalia mkakati, bado hautoshi, commercial farming bado haipo. Huwezi kuleta maendeleo ya nchi kama hakuna commercial farming, huwezi!

Mheshimiwa Spika, sekta hii ambayo tunasema inatoa ajira kubwa, watu wengi are not included. So, kwenye ile tunaita financial inclusion wengi hawapo included. Huwezi kuwa- support mmoja mmoja, lakini kukiwa na kilimo cha kisasa, kukiwa na maeneo au mashamba yametengwa, tukazalisha vizuri, tutatoa ajira nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, lingine ninalotaka kuchangia, nimeona watu wengi wamechangia kuhusu Property Tax, kwa sababu Mheshimiwa Waziri amesema Property Tax sasa itakuwa inakusanywa na Wizara ya Fedha kupitia TRA. Naomba niliweke vizuri. Mheshimiwa Waziri alichosema, hajasema Property Tax yote itakusanywa na TRA. Amesema kwa mwaka huu wanaanza na miji, fedha zitakusanywa na Property Tax na TRA na baada ya kukusanywa ndiyo zitapelekwa sasa, zitarudishwa huko.

Mheshimiwa Spika, huko vijijini bado hawawezi kufika, itakuwa bado ni kazi ya Halmashauri. Hebu tuangalie bajeti ya maendeleo. Maendeleo ya nchi hii tunapozungumzia bajeti ya maendeleo ya nchi hii, maendeleo yanayofanywa na Serikali Kuu yanahusu nchi nzima bila kujali ni wapi. Tumeona sasa hivi flyover zinajengwa pale Dar es Salaam, tunasubiri zije hata huku Dodoma zijengwe flyover maana huku ndiyo Makao Makuu ya Mji, tunahitaji maendeleo nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali inapokusanya, nami naona kabisa kuna logic. Hebu makusanyo haya tuyakusanye mahali pamoja ili tuweze kutekeleza vipaumbele vile ambavyo vitachochea maendeleo ya nchi. Hii kutawanya mapato mara huku, mara huku, ndiyo kunakuwa na wizi na matumizi mabaya ya fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona kwenye Halmashauri yangu kule matumizi ya fedha yalivyo. Makusanyo watu wengi wanaiba. Hata ukiwaambia watumie vifaa vya ki- electronic, wanakuwa navyo lakini hawatumii, wanaiba. Hawa wenye uzoefu wa kukusanya, wakikusanya zikakaa kwenye kapu moja, tutatenga vipaumbele, tutaelekeza kwenye vipaumbele na maendeleo yatakimbia haraka sana, tutaona nchi yetu inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri, ni vizuri, maana uzoefu unaonesha kule kwenye Halmashauri zetu zipo Halmashauri sasa hivi hazina uwezo wa kulipa posho za Madiwani. Fedha hizi zikikusanywa zikaanza kupelekwa kule, watatekeleza miradi ya maendeleo, wataweza kufanya mambo mengine, watalipana hata posho za Waheshimiwa Madiwani, kuliko ilivyo sasa hivi makusanyo hayaridhishi katika maeneo mengi kwenye Halmashauri. Kwa hiyo, naunga mkono hoja, lazima Serikali ikusanye makusanyo pamoja ili yaweze kutoa mchango mzuri na maendeleo ya nchi yaweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kule Jimboni kwangu, ile asilimia 20 inayotakiwa irudi kwenye vijiji, hairudi. Wakikusanya zinatumika hovyo. Hawawarudishii wale wakusanyaji. Usipowa-motivate wakusanyaji, kesho hawawezi kukusanya, nao wanatafuta mbinu nyingine za kuweza kujilipa wenyewe. Kwa hiyo, lazima mikakati iwekwe vizuri ili kuhakikisha kwamba hii fedha inakusanywa na inawekwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, hii Sekta ya Utalii mwaka 2016 tuliweka VAT. Hebu tuangalie, idadi ya watalii waliongia kwenye nchi hii inaonekana wameongezeka, lakini ukiangalia mapato yanayotokana na Sekta ya Utalii, bado siyo mazuri ukilinganisha na nchi jirani kama Kenya.

Mheshimiwa Spika, hii inatupa kwamba kuna mambo lazima tuyafanye kwenye Sekta ya Utalii ili tuweze kuhakikisha kwamba hii sekta inatoa mchango wa kutosha katika kuiendeleza nchi yetu. Naamini tukiweka mikakati mizuri, tukatathmini ile impact ya VAT, maendeleo ya nchi hii yatabadilika kwa haraka sana. Ni muhimu haya mambo yakaangaliwa kwa mapana na marefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, naomba nitamke kwamba naunga mkono hoja na juhudi zote zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuwatetea na kuleta maendeleo ya kweli katika nchi hii. Sote lazima tushikamane; na hivi ni vita, lazima wote tupigane katika kuhakikisha tunaleta maendeleo ya kweli. Hizi tofauti za kisiasa hazitusaidii kutupeleka kokote, hebu tushikamane kuleta maendeleo ya kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza nichukue nafasi hii kuwashukuru wananchi wa Jimbo langu la Vwawa kwa kuniamini na kunichagua kuwa mwakilishi wao katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nawashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchaguliwa na wananchi wa nchi hii na pia Baraza la Mawaziri na viongozi wengine wote ambao wamepewa dhamana ya kuiongoza nchi hii, nawapongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba niupongeze Uongozi wa Bunge, nikitambua kabisa kwamba kazi kubwa tuliyonayo ya Bunge hili ni kuisimamia na kuishauri Serikali. Kama kazi yetu ni kuisimamia Serikali na kuishauri, maana yake kama mambo yatakuwa hayaendi vizuri, basi Bunge hili haliwezi kukwepa wajibu kwamba hatujafanya kazi yetu vizuri ya kuisimamia na kuishauri Serikali. Kwa hiyo, napenda nichukue nafasi hii kuwashukuruni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa kwamba sasa tumepata viongozi wazuri wanaoweza kuikokota na kuisukuma nchi yetu ikafika kuwa nchi ya kipato cha kati. Kwa muda mrefu tulikuwa tunatafuta viongozi, tulikuwa tunatafuta Rais ambaye ana maono ya mbali, sasa Mungu ametupa uwezo, tumebahatika tumepata Rais mwenye maono ya mbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ni tajiri sana kwa kuwa na ardhi nzuri yenye rutuba, ambayo imejaa karibu kila kona. Tuna madini ya kila namna, tuna misitu, tuna mlima mrefu kuliko milima yote katika Afrika na wa pili duniani kwa urefu, tuna mbuga nyingi za wanyama, mito, maziwa, bahari na zaidi ya hapo tuna watu zaidi ya milioni 53. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni competitive advantage ambayo tunayo. Kwa maana hiyo, tuna vitu vingi vinavyoweza kuiwezesha nchi yetu kuendelea na kufika kuwa nchi ya kipato cha kati. Sasa tatizo kwa muda mrefu limekuwa ni nini? Tatizo kubwa ni tatizo la uongozi na hili ndio limekuwa likitusumbua sana. Sasa wakati huu tumepata viongozi, nadhani tutaweza kwenda vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa Fedha kwa kuleta Mpango huu na kueleza dira na kuonekana mambo ambayo tunaweza kuyafanya. Mpango huu umezingatia dira ya Taifa na pia umezingatia Hotuba ya Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania. Napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, naomba nichangie katika eneo la kilimo. Katika Mpango huu kilimo bado hakijapewa nafasi nzuri sana na hakijapewa mkazo kama ambavyo kingekuwa kimepewa. Sisi kule Wanavwawa ni wakulima, wananchi wa Vwawa wanalima sana, tunalima kahawa kwa wingi, mahindi, tunalima mazao mengi na tunaamini kabisa kama Serikali itatuwekea misingi mizuri, ikatupatia pembejeo kwa wakati, tuna uwezo wa kuzalisha chakula kwa kingi ambacho kinaweza kikatumika sehemu nyingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe wazo kwamba tusiseme mazao ya biashara, sasa kila zao ni zao la biashara, hata mahindi ni zao la biashara, hata maharage ni zao la biashara. Kwa hiyo, mazao yote yanayoweza kulimwa yapewe uzito unaostahili ili tuweze kuzalisha chakula kingi, tuweze kuzalisha kwa ajili ya kuuza sehemu zinginezo. Kwa hiyo, kilimo ni muhimu sana tukakipa uzito unaostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili, ambayo ningependa nichangie, tumezungumzia viwanda, kwamba Serikali ya Awamu ya Tano itakuwa ni Serikali ya viwanda. Hata hivyo, viwanda ambavyo tumesema, nimesoma kwenye huu Mpango hatujaainisha, tunataka viwanda vingapi na viwe wapi? Hilo hatujalisema, lakini pia tulikuwa na viwanda vingi sana ambavyo vilijengwa katika nchi hii, nini kilitokea viwanda hivyo vyote vikafa? Tulikuwa na mikakati mingi ambayo tuliweka juu ya viwanda, tumejifunza nini katika mipango yote tuliyokuwa nayo katika kujenga viwanda vilivyopita? Sasa haya yanatakiwa yawe ni msingi mzuri wa kutuwezesha kuweka mikakati mizuri ya kuweza kujenga viwanda tunavyovihitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ili tuweze kwenda sambamba kufika kwenye hiyo nchi ya viwanda, tunahitaji viwezesha, vitu vitakavyotuwezesha kufika huko, tunahitaji umeme, barabara na vitu vingine vingi. Sasa naomba nichangie kwenye suala la umeme; umeme wa REA umesambazwa nchi nzima katika vijiji vingi sana. Katika Jimbo langu kule watu wengi wamepata, lakini vijiji vingi bado havina umeme. Kuna Vijiji kama Nanyara, Nswiga, Irabii umeme unapita juu kwa miaka mingi, unawaruka wananchi unakwenda wapi, wananchi wale wanahitaji wapate ule umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nasema kwamba umeme ni muhimu sana na Mheshimiwa Waziri wa Nishati ameona kule kuna joto ardhi, kule kuna chanzo kizuri sana cha kuweza kuzalisha umeme. Naomba mkazo uwepo katika kuanzisha na kutumia nishati hii inayotokana na joto ardhi ambayo inaweza ikatusaidia sana kutukwamua katika suala hili la umeme ambalo ni muhimu sana katika kuipeleka nchi kuwa nchi ya kipato cha kati.
Suala lingine ambalo ningependa kuchangia, ili tuweze kuwa nchi ya kipato cha kati, tunahitaji wataalam wetu, tunahitaji watu wawe na ujuzi wa kuweza kufanya kazi na kuweza kutekeleza majukumu yetu. Sasa hivi vyuo vyetu tulivyonavyo na mfumo wa elimu tulionao, hauwaandai vijana kuweza kupata ujuzi unaohitajika sokoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, tunayo kazi kubwa ambayo napenda nishauri, Wizara ya Elimu tutafakari kwa undani mitaala tuliyonayo inatuandaa, inawaandaa vijana wetu kwenda kuwa nchi ya kipato cha kati? Sasa hivi mkazo utatiliwa kwenye Vyuo vya Elimu ya Juu. Naomba nishauri, lazima tuwe na vyuo vingi vinavyotoa elimu ya kati tertiary institutions ambazo zitatoa wataalam watakaoweza kushiriki kufanya kazi katika viwanda tunavyovihitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kwenye upande wa elimu, ningependa mitaala ile wakati inaandaliwa, iandaliwe vizuri, iwe ni demand driven rather than supply driven, halafu wapatiwe sehemu za kwenda kufanya field ili waweze kuiva na kukomaa hilo litatusaidia sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka haraka naomba nishauri mambo mengine yafuatayo:-
Kwanza, ili tuweze kufika na kutekeleza mpango huu ambao ni mzuri, nashauri, lazima tuweke nguvu sana katika ukusanyaji wa mapato, bila kukusanya mapato huu Mpango utakuwa hautekelezeki. Sasa hivi lazima tuweke mkakati wa kutosha wa kuhakikisha kwamba nchi inajitegemea kimapato kuliko kutegemea wafadhili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, tubadilike kifikra ili watu watambue kwamba wajibu wa maendeleo ya nchi hii ni sisi wenyewe ndiyo tutakaoleta maendeleo, ni wananchi wa nchi hii ndiyo watakaoleta maendeleo na si mtu mwingine.
La tatu, naomba kushauri, tumekuwa tukiimba kila wakati kwamba huko vijijini wananchi wanahitaji huduma za fedha, bila kupeleka huduma za fedha, bila kuanzisha hizi micro-institutions za kuweza kuwa-support wakulima, ku-support watu mbalimbali huko vijijini, ku-support vikundi mbalimbali, hatuwezi kuleta maendeleo ya kweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri tuimarishe huduma za fedha mpaka vijijini ili wananchi wetu waweze kupata mikopo mbalimbali na kugharamia vitu mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho napenda pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha ni vipaumbele, tunahitaji tuwe na vipaumbele vichache, ambavyo vitagharamiwa na Serikali. Viwanda naamini vitagharamiwa vitakuwa vinaendeshwa na watu binafsi siyo Serikali tena. Sitegemei kuona Serikali inaweka mkono mkubwa wa kuendesha viwanda wakati uwezo wetu ni mdogo, labda viwanda vile ambavyo ni strategic, lakini viwanda vitaendeshwa na private sector. Katika maeneo ya elimu, kilimo, uvuvi na ufugaji, afya na maji, miundombinu, barabara, viwanja vya ndege, umeme; hivyo Serikali lazima iwekeze vizuri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba nishauri tumezungumzia sana kwamba tunahitaji viongozi ili waweze kuisukuma nchi hii. Hata hivyo, katika nchi hii hatuna utaratibu wa kuandaa viongozi, wala wa kuwafundisha, wala kuwaelekeza namna ya kutekeleza majukumu yao.
Sasa umefika wakati tuwe na mfumo mzuri wa kutambua viongozi wazuri na kuwaendeleza na kutambua vipaji vyao ili wakabidhiwe kufuatana na uwezo walionao. Hilo litatusaidia kuwa na viongozi wanaoweza kujenga, wazalendo wenye uwezo wa kuleta maendeleo ya kweli katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nashukuru sana na pia naomba Serikali izingatie mawazo yetu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JAPMheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni hifadhi ya jamii. Kwa kuwa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi iliazimia kuanza kuwalipa pensheni wazee wote waliofikia umri mkubwa bila kujali walikuwa waajiriwa au laa, je, ni lini hasa ahadi hii ya kulipa pensheni kwa wazee hawa ambao wanaisubiri sana itatekelezwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ni kwa lini Sera ya Hifadhi ya Jamii itaanza kutekelezwa kwa wananchi wote yaani wakulima, wafanyakazi, wafanyabiashara ili kila mwananchi afaidi mafao ya hifadhi ya jamii? Pia kuna mkakati gani wa kupunguza malalamiko ya wananchi ambao husumbuliwa sana na Mifuko ya Jamii kama NSSF na PPF? Je, hatua za kuboresha mifumo hii zimechukuliwa vipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, sekta binafsi. Hivi sasa sekta binafsi ndiyo mhimili mkuu wa kukuza uchumi wa nchi yetu ikiwa ni pamoja na kutoa ajira kwa wananchi wengi zaidi. Hata hivyo, waajiri wengi wa sekta hii hususani kilimo, ulinzi, huduma za hotelini, biashara na viwanda wamekuwa hawatoi mikataba na barua za ajira na wakati mwingine masharti ya kazi ni magumu sana na ya kinyonyaji, mazingira yanatisha sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia baadhi ya waajiri hulipa mishahara duni ambayo haiendani na uzalishaji na haina tija. Lazima Serikali ihakikishe kwamba waajiri wote wanakuwa na mikataba na barua za ajira zinatolewa kwa wafanyakazi wote. Hili liende sambamba na kuimarisha Idara ya Kaguzi za Kazi ili ifanye kazi ya ukaguzi mara kwa mara na kutangaza hadharani waajiri ambao wanakiuka sheria za kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, Serikali kuboresha kilimo. Ni lazima Serikali ije na makakati mpya wa kuinua kilimo ikiwa ni pamoja na kuboresha mfumo wa ruzuku, usambazaji wa pembejeo, masoko, chakula, kama vile kahawa, mahindi, maharage na kadhalika. Je, Serikali imefanya uchambuzi ili kuimarisha kilimo kwenye maeneo yenye tija na kujenga mazingira wezeshi ili kuongeza thamani ya mazao? Nashauri pale ambapo wananchi wanaweza kuuza nje mazao yao waruhusiwe kwani itasaidia kuongeza fedha za kigeni. Pia mkakati wa kuanzisha kilimo kikubwa ili kutoa ajira kwa vijana wetu umefikia wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ni mkakati wa kuanza kutengeneza magari na vipuli. Serikali lazima ifanye maamuzi magumu ya kimkakati ili kuanzisha kiwanda cha kutengeneza magari na vipuli vyake. Kiwanda hiki kitasaidia kuchukua vijana wetu wengi ambao wana ufundi mkubwa. Kuna mafundi wazuri katika mikoa yetu. Ni muhimu kuanza kutengeneza magari ambayo yatatumia gesi na mafuta. Pia itasaidia kufanya utafiti na kuziangalia projects za wanafunzi wa vyuo vya ufundi ambazo ni nzuri sana. Maamuzi haya ni muhimuHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kwenye maeneo yafuatayo:
sana ili kutoa ajira na kuokoa fedha za kigeni zinazotumika kununulia magari na vipuli.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utakuwa katika maeneo yafuatayo:-
Kwanza, mafunzo ya awali kwa Watumishi wa Umma. Serikali ihakikishe kwamba waajiriwa wote katika Utumishi wa Umma wanapoajiriwa kwa mara ya kwanza wanapatiwa mafunzo elekezi katika maeneo mbalimbali kama vile, uwajibikaji, maadili, OPRAS, Sheria, Kanuni na miongozo mbalimbali. Bajeti ya mafunzo ipelekwe Utumishi ili Chuo cha Utumishi kitoe mafunzo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile viongozi wanaoteuliwa katika ngazi mbalimbali wapewe induction na orientation ya majukumu yao ya kusimamia rasilimali watu, fedha na mali za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ni suala la OPRAS, lazima ifike mahali Serikali kuanza kuwachukulia hatua watumishi ambao hawajazi fomu za OPRAS. Pia Taasisi zisizofanya vizuri na zinazofanya vizuri, katika kutekeleza OPRAS zitangazwe hadharani ili wananchi wote wajue. Sanjari na hilo vigezo vya kupima taasisi mbalimbali vitayarishwe na kuanza kutumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, ni fedha za TASAF awamu ya tatu katika baadhi ya maeneo; fedha hizi zinalipwa kwa wasiohusika kama pale Vwawa Mjini na baadhi ya vijiji, hebu fanyeni uchambuzi vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nnem ni usimamizi wa malipo ya mishahara; kuna haja ya kuongeza jitihada za kusimamia mfumo wa mishahara (Lawson version 9), bado Watumishi hawaitumii sawa na kusababisha ucheleweshaji wa malipo kwa baadhi ya watumishi. Waajiriwa wapya ni waathirika sana wa hili. Pia watu wanaoachishwa kazi na kustaafu kazini.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tano, ni kuboresha miundo ya Utumishi katika Kada mbalimbali. Hivi sasa miundo ya Kada nyingi imepitwa na wakati, lini mtaanza kuipitia upya miundo hiyo? Pia taasisi nyingi zimekuwa zinaanzishwa bila kuwa na miundo ya Taasisi husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la sita, ni kuhusu Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania. Kwa kuwa, Chuo hiki kilianzishwa ili kutoa mafunzo ya Uongozi, Menejimenti na Utawala Serikalini, je, ni lini hasa Serikali itaanza kukitumia Chuo hiki ipasavyo ili kitoe mchango unaohitajika katika kujenga rasimali watu iliyotukuka. Sanjari na hilo Chuo kinategemea kufundisha Watumishi wa Umma wangapi katika mwaka wa fedha 2016/2017. Pia ningependa kujua tafiti ngapi na katika maeneo yapi chuo kimepanga kufanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa ufafanuzi mbele ya Bunge lako tukufu kuhusu baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wa kujadili hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2018/2019.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia afya njema ya kuwa hapa kwenye Bunge lako tukufu kujadili bajeti ya Serikali. Aidha, nachukua fursa hii kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile namshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Mbunge na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa miongozo wanayoitoa katika kuendeleza na kuboresha uhifadhi nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kukupongeza wewe mwenyewe na Naibu Spika kwa kuliongoza vyema Bunge letu la Kumi na Moja katika Awamu ya Tano ya uongozi wa nchi yetu.

Aidha, kwa namna ya pekee napenda kuipongeza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Nape Moses Nnauye na Makamu wake Mheshimiwa Kemilembe Julius Lwota na Waheshimiwa Wajumbe wote kwa namna ambavyo wameendelea kuishauri Wizara yetu ili kuimarisha sekta ya maliasili na utalii ifikie dira na dhima yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba kuchukua nafasi hii kuishukuru sana familia yangu na watoto wangu ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakiniombea, wakinishauri na kunipa faraja katika kipindi chote ambacho nimekuwa nikifanya kazi hii kama Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nichukue nafasi hii kukishukuru chama changu, Chama cha Mapinduzi, Kamati ya Siasa ya Wilaya ya Mbozi kwa jinsi ambavyo wamekuwa wakinisaidia katika kutekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, nawashukuru sana wapiga kura wa Jimbo la Vwawa kwa muda mrefu wamenikosa na wamekuwa hawana muda wa kutosha wa kukaa na mimi, lakini naomba niwaambie kwamba nipo pamoja nao na ninaendelea kutekeleza majukumu ya kitaifa na wao waendelee kutekeleza majukumu yale mpaka hapo Mungu atakapopenda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamechangia katika kuboresha bajeti yetu hii. Kwa kweli niseme Waheshimiwa Wabunge wametoa michango mizuri sana. Michango yao inafaa sana na kwa kweli kama tutaweza kuitumia michango yote hii ni imani yangu kabisa tutaboresha uhifadhi na tutaboresha utalii wetu katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu muda ni kidogo sana, hatutaweza kutoa ufafanuzi wa hoja zote zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Naomba nichukue nafasi hii kutoa ufafanuzi wa hoja chache ambazo Waheshimiwa Wabunge wamechangia.

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ufafanuzi mzuri ambao ameutoa juu ya migongano, sheria na kama sheria zilivunjwa na kadhalika. Pamoja na Waziri wa Katiba na Sheria kwa jinsi ambavyo wamefafanua hoja mbalimbali, kwa kweli tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na sekta ya uwindaji wa kitalii; kumekuwepo na hoja nyingi sana zinazohusu juu ya uwindaji wa kitalii. Wapo Waheshimiwa Wabunge ambao kwa undani kabisa na kwa dhati wamechangia vizuri sana na wengine wakasema hii biashara sasa imedorora ni kwa sababu labda hatua ambazo zimechukuliwa hazikuzingatia sheria. Naomba niseme kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, biashara ya uwindaji wa kitalii inaongozwa na sera, sheria, kanuni na miongozo mbalimbali ambayo Serikali imeiweka na hiyo ndiyo inayotu-guide namna ya kuendesha uwindaji wa kitalii nchini. Katika Sheria Namba 5 ya mwaka 2009 na Kanuni zake za mwaka 2015 zinatoa namna ya uwindaji wa kitalu utakavyoendeshwa kwenye nchi hii, namna vitalu vitakavyogawanywa na vitalu vingapi vitakuwa ni vya wenyeji, labda ni makampuni mangapi ya nje yatakuwepo? Kwa hiyo, sheria ile inafafanua vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na hoja kwamba mnamo mwezi Oktoba, 2017 Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii ilibadili utaratibu wa kugawa vitalu kutoka kwenye ule utaratibu wa zamani wa kiutawala (administrative allocation) kuelekea kwenye mfumo mpya wa mnada. Kwa nini wakasema kwamba kumekuwa na ukiukaji wa sheria?

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kusema kwamba kwanza ni kweli kabisa makampuni ya uwindaji yalipewa kibali cha kufanya uwindaji kwa miaka mitano kuanzia mwaka 2018 mpaka mwaka 2022. Wakati wanapewa hiyo mikataba ya miaka mitano, kwenye barua kulikuwa na maelekezo mazuri kabisa ambayo yalisema kwamba kufuatia mageuzi yanaoendelea ndani ya Wizara katika kuimarisha Sekta ya Uwindaji wa Kitalii, Waziri mwenye dhamana ya Maliasili na Utalii anaweza kubadilisha wakati wowote na imeandikwa na kufafanuliwa vizuri kabisa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kutafakari namna sekta ya utalii ambavyo imekuwa ikiendeshwa nchini, tuliridhika kabisa kwamba bado kuna upungufu ambao upo ambao ni lazima tuurekebishe ili uendane na hali halisi iliyopo kwa sasa. Moja ya sababu iliyowekwa katika ile barua ya mkataba wa awali, ilikuwa ni kwamba kwa sasa hivi vitalu vya uwindaji viko chini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA), lakini TAWA ndiyo inaanzishwa na kwa sababu ndiyo inaanzishwa, itakuja sasa na utaratibu mpya wa namna ya kusimamia hivyo vitalu, ndiyo maana kulikuwa na hicho kigezo kwenye ile barua.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa kuangalia kile kigezo ndiyo maana tukaamua kwamba sasa hebu tusitishe ili tuje na utaratibu mzuri kabisa ambao utakuwa na manufaa makubwa mawili; kwanza utaongeza mapato ya Serikali kwa sababu sasa tutafanya kwa mnada. Kwa hiyo, badala ya vile vitalu vingine kuuzwa labda dola 5,000, dola 15,000 na dola 30,000; vile vya daraja la kwanza kuuzwa dola 60,000, sasa unaweza ukakuta baadhi ya vitalu vikauzwa mpaka hata dola 300,000. Kwa hiyo, tukaona Serikali itapata mapato makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana tukasema sasa lazima hili tulifanyie marekebisho ili liendane na kwanza na tamko ambalo lilikuwepo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwamba vitalu vya uwindaji vitaendeshwa kwa njia ya uwazi na kwa njia ya mnada ili kusudi kusiwe na milolongo ya rushwa na nini, watu waamue wenyewe na wapange bei wenyewe. Basi tukaona kwamba hili ni la msingi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusitisha, wadau wa uwindaji walitoa malalamiko yao wakatuambia hii sasa mta- frustrate industry, na sisi tukaa tukakubaliana, tukasema kweli kuna hoja. Walipotueleza tukaelewa na ndiyo maana tukasema sasa wakati tunakwenda badala ya kwamba tusitishe mwezi wa kumi ule halafu mwezi wa kwanza tuwe tumetoa, tutashindwa. Ndiyo maana tukaamua kufanya extension ya ule muda wa kwanza, tukaongeza miaka miwili wakati haya mabadiliko sasa yanaendelea kufanyika. Ndiyo maana wamepewa tena wameongezewa miaka miwili. Wameongezewa katika ile baada mitano baada ya kumalizika, wameongezewa miwili. Katika kipindi hiki, Serikali sasa itakuja na utaratibu mpya wa namna ya tutakavyoendeshwa kwa minada.

Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na hoja kwamba baada ya kutangaza hivi, kuna matatizo yamejitokeza; wakasema vitalu vingi vimerudishwa. Naomba nilitaarifu Bunge lako tukufu kwamba sekta ya uwindaji wa kitalii sasa hivi inakabiliwa na changamoto nyingi sana hapa, siyo tu kwa Tanzania bali kwa dunia nzima. Kuna mambo mengi yanaendelea katika hili. Kwanza wawindaji wa kitalii ni kweli kabisa ni wale wale ambao wapo nchi zote, ukiwa-frustrate hapa watahamia kwingine. Kwa hiyo, ni kweli lazima tuwalinde vizuri.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kuna kampeni zinaendelea duniani, kuna watu wanaosema wanalinda haki za wanyamapori. Hawa wamekuwa wakifanya kampeni kila mahali kwamba kuwinda wanyama ni dhambi kubwa. Hizo kampeni za anti-hunting zinaendelea. Makampuni mengi duniani sasa hivi yanafanya kampeni. Kwa hiyo, hiyo kwa kiwango fulani imeathiri kushuka kwa biashara ya uwindaji wa kitalii. Hiyo ni sababu ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sababu ya pili, baadhi ya nchi ambazo ndiyo wadau wakubwa wa uwindaji wa kitalii zimepiga marufuku baadhi ya trophy ambazo zilikuwa zinaenda ikiwemo Marekani na nchi za Ulaya (European Union) zimepiga marufuku na baadhi ya nchi juzi juzi tumesikia hata China wamepiga marufuku. Kupiga marufuku kule kutaathiri moja kwa moja biashara ya uwindaji wa kitalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sababu ya tatu, sheria yetu ile ilikuwa inasema asilimia 85 lazima ziwe ni kampuni za wazawa na lengo lilikuwa ni kuwasaidia wazawa ili waweze kumiliki hizi kampuni na wapate mapato makubwa kusudi wageni wawe na asilimia 15 tu ya makampuni. Ni kweli ilikuwa ni sheria nzuri na wazawa wengi walichukua, walipata hii, lakini kutokana na changamoto za biashara hii, kampuni nyingi za kizawa zimeshindwa kufanya hii biashara, ndiyo maana zikafikia hatua ya kuanza kuzirudisha.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa mpaka sasa hivi ni vitalu 81 vimesharudishwa, vimekosa wawekezaji. Huko nyuma baadhi ya makampuni yalikuwa yanunue hivi vitalu halafu tena yanavikodisha kwa Wazungu. Sasa hivi hiyo biashara haipo. Na sisi tunataka kwamba wale wale wanaokodi, wenyewe wazingatie sheria, sera unaendesha wewe mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hilo, ndiyo maana sasa kumekuwa na kushuka kwa hii biashara ya wenzetu. Kwa hiyo, ndiyo maana vitalu vingi vimerudishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tulichokifanya, sasa hivi tunaendelea kuuandaa utaratibu, mojawapo, vitalu hivi 81 vilivyorudishwa navyo pia tutaviingiza kwenye huu mnada ambao utakuja ambao tutautumia kusudi watu waweze kufanya hivyo. Pia katika hilo lazima tuendane na sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa na hoja kwamba baada ya wale wawekezaji waliokuwa kwenye vile vitalu walipoondoka kuna changamoto zimejitokeza. Watu wakasema vitalu vimebaki bila ulinzi, bila nini.

Mheshimiwa Spika, naomba kulitaarifu Bunge lako tukufu kwamba wale wawekezaji wakati wanaendesha au wanamiliki vile vitalu na Serikali pia tulikuwa bado tuna watumishi wetu wanaoshirikiana na zile kampuni za ulinzi. Baada ya wale kuondoka, sasa hivi tunabaki sisi wenyewe tunaendelea kulinda.

Mheshimiwa Spika, pia katika kile kikosi maalum cha Kitaifa ambacho kilianzishwa, yaani kile ambacho tumekuwa tukizunguka nchi nzima, wamekuwa wakipambana na uwindaji haramu, basi kampeni hiyo imefanyika vizuri na ulinzi umefanywa vizuri hasa kwa kutumia intelijensia. Sasa hivi matukio ya ujangili yamepungua kwa kiwango kikubwa sana. Kwa hiyo, vile vitalu vingi vipo salama na Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba inavilinda hivyo vyote ili viwe na manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunadhani hata baadhi ya yale mapori ya akiba, Mheshimiwa Waziri atayasemea, tunafikiria yapandishwe hadhi kama baadhi ya Waheshimiwa walivyosema, yaende kufikiwa kuwa ni Hifadhi za Taifa, yakifika hapo tutakuwa tumefikia hatua nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine kutokana na changamoto hizi ambazo zinaendelea duniani, tunataka tuanze kuipunguza hii biashara ya uwindaji wa kitalii, tuanze kwenda kwenye utalii wa picha zaidi. Utalii wa picha zaidi utaleta manufaa makubwa na utalinda hata hizo haki za wanyamapori kama ambavyo watu wengine wamekuwa wakisema.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana katika baadhi ya maeneo na katika mradi ambao tunakuja nao ule wa kuinua utalii wa Kusini (Regrow) ambao unahusu mbuga ya Selous, Mikumi, Udzungwa na Ruaha ambao tunaanza nao, kwa asilimia kubwa tunataka tuhakikishe hata kule Selous, Kanda ya Kaskazini tulete utalii wa picha badala ya utalii wa uwindaji kusudi tuweze kupata mapato makubwa. Ninaamini kabisa hiyo itasaidia sana katika kuleta hayo manufaa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilitaka tu nitoe ufafanuzi huo kwamba yale ambayo tuliyafanya, tuliyafanya kwa mujibu wa sheria na kwa sababu barua, au mkataba wenyewe ulikuwa una-provide ndiyo maana hayo yalifanyika.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo ningependa kutoa ufafanuzi kidogo ni kuhusu sekta ndogo ya misitu. Waheshimiwa Wabunge, wamezungumzia mambo mengi sana kuhusiana na sekta ya misitu na mambo mengi. Kwa kweli nawashukuru sana na niwapongeze. Ni ukweli usiofichika kwamba sekta ya misitu ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi hii. Misitu inachangia asilimia nne.

Mheshimiwa Spika, hebu tuangalie jinsi misitu yetu inavyosimamiwa, kuna Serikali Kuu; Serikali Kuu ina hifadhi 455, lakini kuna nyingine ziko chini ya Halmashauri kama 167; lakini Serikali za Vijiji zina hifadhi 1,200. Sasa unapokuwa na hifadhi ambazo ziko scattered, zina mamlaka tofauti, lazima kuwe na changamoto. Ndiyo maana tukaamua sasa kupitia upya sera ya misitu ili hii sera ikipitiwa upya, ikihuishwa, tulete sasa sheria ambayo itahakikisha kwamba hii sekta ya misitu inatoa mchango mkubwa sana katika uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hiyo basi, ndiyo maana kuna mapendekezo, hata Kamati nafikiri imependekeza kwamba tuwe na mamlaka moja. Waheshimiwa Wabunge, nawashukuru sana kwa hiyo hoja. Tuwe na mamlaka ya kusimamia misitu yote Tanzania. Hii itatusaidia sana. Misitu ndiyo uhai, bila misitu hakuna maji, bila misitu hakuna maisha na kwenye sekta hiyo ndiyo tuna nyuki, tuna asali, tuna vitu vingine vingi tu.

Mheshimiwa Spika, naomba niliambie Bunge, sasa hivi kwenye sekta ya nyuki hatujaiendeleza, lakini tunaamini tutaiendeleza vizuri sana. Mkitupa fedha tutaiendeleza sekta hii vizuri. Kwa sababu kwenye nyuki pale, najua hata baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hawajui, nyuki wanatoa maziwa ambayo ni mazuri sana. Pia kwenye nyuki pale tutapata nta, asali na mambo mengi sana, soko ni kubwa. Uzalishaji wa asali ukiongezeka, nta ikiongezeka, maziwa yakiongezeka na baadhi ya kemikali ambazo zinatokana na mazao haya, kutasaidia sana katika kuleta fedha kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine lililojitokeza katika upande wa misitu ni matumizi ya mkaa. Waheshimiwa Wabunge wengi wamelalamika kwamba kweli sijui kuna sehemu wanakamatwa, mikaa inazuiwa, mikaa imefanya nini; naomba nilitaarifu Bunge lako tukufu kwamba sisi tulichokifanya, hatujazuia matumizi ya mkaa. Tunasema kwa sababu asilimia kubwa ya Watanzania wanatumia mkaa, basi lazima tuwe na utaratibu mzuri wa maeneo ya upatikanaji wa mkaa. Tukiruhusu kila mahali kila mtu anauza mkaa, kila mtu anavuna, basi hiyo inakuwa ni changamoto katika uhifadhi wa misitu yetu.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana sasa tunasema kwamba tunataka wananchi wapewe elimu, wawe na meko yanayotumia mkaa kidogo. Pia tuwe na centres ambazo zina vibali wamelipia tozo zinazostahili, tuwe tunajua kwamba wanauza mkaa. Tatu, tuje na elimu. Sasa hivi tumefanya utafiti tumegundua kuna baadhi ya miti ambayo tutahamasisha ipandwe kila mahali ambayo inachukua kati ya miaka mitatu na minne, inafaa sana kwenye kuni na inafaa sana katika uzalishaji wa mikaa. Kwa hiyo, hiyo misitu nayo tutaisambaza, elimu hiyo tutaitoa ili wananchi wa nchi hii wahamasishwe namna ya matumizi bora ya hizo kuni na mikaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala ambalo limejitokeza kwamba boda boda wanakamatwa kila mahali wakiwa wamebeba mkaa, magari yanakamatwa; nataka niseme hivi, kwa mujibu wa Sheria ya Usalama Barabarani, bodaboda hawaruhusiwi kubeba mkaa. Hawaruhusiwi kwa mujibu wa sheria, yale hawaruhusiwi kabisa! Kwa hiyo, tunachosema, magari yaliyoruhusiwa yenye vibali ndiyo hayo yaweze kuruhusiwa kusambaza mkaa katika vituo mbalimbali na wananchi waelekezwe wapi mkaa halali unapatikana ili wale wanaochukua kwa rejareja wachukue katika hayo maeneo.

Mheshimiwa Spika, naamini kwamba hilo litapunguza changamoto ambazo zipo katika suala hili la matumizi ya mkaa. Ni muhimu sana wananchi wakaelimishwa matumizi ya mkaa vizuri, tuwe na majiko mazuri, tuwe na namna ya kuendeleza hii sekta, itatusaidia sana katika maisha yetu na itatoa mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, viwanda vingi vinavyotokana na misitu; sasa hivi tuna viwanda vingi vinatokana na mazao ya misitu. Ni imani yangu kabisa kwamba hii Sekta Ndogo ya Misitu lazima tuiimarishe ili vile viwanda vyote vitoe mchango mkubwa kwa sababu Sera yetu ya Taifa inataka tuwe ni nchi ya viwanda. Sasa viwanda vinavyotokana na mazao ya misitu lazima viimarishwe na vihakikishe kwamba kwa kweli vinatoa mchango ule unaohitajika.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja kwamba baadhi ya watumishi katika maeneo ya hifadhi wamekuwa wakitoa rushwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwanza kwa kunipa hii nafasi, lakini nichukue nafasi hii pia kuwashukuru Wabunge wote ambao kwa namna moja ama nyingine mmechangia katika taarifa ya Kamati hii. Pia naomba niunge mkono taarifa ya Kamati zote mbili, lakini kipekee niwapongeze Wajumbe wa Kamati ya Kilimo. Ripoti yao imesheheni mambo mengi mazuri na ya msingi sana ambayo sisi kama Serikali tutayafanyia kazi na tutaona namna ya kuweza kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge hawa ili tuweze kufikia hii azma ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee namshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na Viongozi wengine wote Wakuu pamoja na Mawaziri kwa kuendelea kukiunga mkono kilimo cha nchi hii. Hapa Waheshimiwa Wabunge wote naomba mniunge mkono kwa sababu ningi wote ni wadau wa kilimo. Kama muda ungetosha, najua mngepata nafasi ya kuzungumza. Wote hapa ni wadau wa kilimo, wote hapa tumekula chakula ndiyo maana tunaongea. Kwa hiyo, wote kwa namna moja ama nyingine ni wadau wa kilimo.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingi zimetolewa, lakini naomba nianze kwa hoja chache, bahati mbaya naona Mheshimiwa Zitto hayupo, lakini naomba nianze na hii hoja yake. Hoja ya kwanza ambayo ameisema, ni kuhusu chanzo cha fedha ambacho Benki yetu ya Kilimo imepata, labda naomba niweke takwimu vizuri, siku fulani hapo juzi nilisema, Benki yoyote duniani inayoitwa Benki ya Biashara, benki yoyote inategemea mitaji yake katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kuna mtaji unaowekeza na wenye hisa na ukiangalia mtaji wa wenye hisa, ni mtaji ambao unawekezwa na ule mara nyingi ni kwa sababu ya taratibu za kibenki inakuwa kama dhamana; na mara nyingi unawekwa Benki Kuu. Benki baada ya kuanzishwa, iki-comply na zile taratibu za kuanzishwa, inatakiwa itafute fedha mahali popote zilipo nyingi ilete iweke na ipeleke mahali zinapotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano, nianze na CRDB. Ukichukua mtaji wa CRDB wa wenye hisa, ni shilingi bilioni 65,296; lakini angalia mali walizonazo, wana mali zaidi ya shilingi trilioni 6,038,571. Wana shilingi trilioni sita, mtaji shilingi bilioni 65. Kwa hiyo, pale siyo kwamba wanafanya biashara kwa kutumia hela za mtaji, kazi yao ni ku mobilize fedha kutoka ziliko, wanakuja kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukichukua NMB, wana mtaji wa shilingi bilioni 20, lakini angalia mali zao walizonazo; asset za NMB ni zaidi ya shilingi trilioni tano. Ni shilingi trilioni 5,706,110. Kwa hiyo, ina maana hawa wanafanya kazi ya biashara. Vivyo hivyo Benki yetu ya Kilimo, ina mtaji mkubwa kuliko hata NMB. Benki yetu Serikali iliwekeza shilingi bilioni 60, nayo inaendelea kufanya kazi na kutafuta fedha na kuendesha na tunataka hii benki iendelee kutoa mikopo kwa wakulima wa nchi hii ili kilimo kiweze kusonga mbele.

MBUNGE FULANI: Shule hiyo!

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa kuanzia ndiyo maana benki hii imetafuta fedha. Ilikopata mimi sijui, imetafuta. Ninachokijua, wametoa fedha kwenye Bodi yetu ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko. Wametoa mkopo; na mkopo lazima ulipwe. Bodi yetu inalipa. Tumekopa Benki ya Kilimo ambayo kazi yake ni kufanya biashara.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme kwamba kazi yetu sisi ni kukopa na hiyo Bodi yetu ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko imekopa, inaendelea kukopa, inafanya biashara, imenunua korosho, kazi yake ni kununua, kuchakata na kwenda kuziuza hizo korosho. Hiyo tutaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu nilotaka kulizungumzia na bahati nzuri amesema Mheshimiwa Zitto na Waheshimiwa Wabunge wengine wamechangia, naomba niseme, Serikali yoyote duniani iko pale kwa mujibu wa Katiba na kwa mujibu wa sheria.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tusikilizane. Hii ni shule, msikilize vizuri. (Makofi)

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kazi ya Bunge ni kutunga sheria. Sheria hizo zikishatungwa, kazi ya Serikali ni kuzitekeleza hizo sheria. Sasa mwaka 2009, Bunge lako Tukufu lilitunga sheria inayohusu Zao la Korosho. Ilipotunga sheria, iliweka vifungu mbalimbali. Kwa sababu ya muda, naomba niweke vizuri ili tuelewane. Ukisoma hiyo Sheria ya Bodi ya Korosho, Kifungu cha 12 (1) kinasema hivi: “every cashew nut dealer, being a buyer, processor, importer, exporter, wherehouse owner or operator shall be required to register with the Board.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mtu yeyote anayegusa, anayeshughulika na korosho kwa namna yoyote ile, lazima kwanza aandikishwe na Bodi. Ukisoma Kifungu cha 15(4) kinasema hivi: “a person shall not buy,” naomba Mheshimiwa Zitto uishike vizuri. “A person shall not buy, sell, process, own or operate a wherehouse or exports any cashew nuts on commercial basis without a licence issued by the Board.” Huu ndiyo msingi ambao tunautumia sisi kusimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, unapokuja na hoja unasema sijui kuna Kangomba sijui wafanye nini, mwaruhusu, kazi yako ya kwanza kama Mbunge, itisha turekebishe hii sheria. Kama hatujarekebisha, sitaisimamia hii. Kama unataka korosho zinazotoka nje, zinazotoka popote zije, zifuate utaratibu ulioandikwa kwenye sheria. Kwa hiyo, huo ndiyo msimamo ambao sisi kama Serikali tutaendelea kuusimamia na tutaendelea kuhakikisha kwamba haya yote yanazingatiwa.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia kuhusu kilimo, nami nakubaliana kabisa. Zipo hoja za msingi mlizosema namna ya kuboresha kilimo chetu. Kilimo chetu hiki ili tuweze kukiboresha vizuri, jambo la kwanza ambalo lazima tuangalie ni mifumo yetu ya pembejeo nchini. Hilo nakubaliana na Kamati imetoa maoni, imeshauri, tutayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, inaendana na tija; ni ukweli usiofichika. Kwenye kilimo chetu, tija bado iko chini. Ukiangalia tija bado iko chini; ukiangalia upatikanaji wa mbegu bora, bado hata hatujakaa vizuri. Hili ndiyo suala tunalolifanyia kazi. Pembejeo viuatilifu na madawa mengine hivi vyote ndiyo msingi, lakini pia kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, watu wetu katika maeneo mengi, ukiangalia mashamba tunayolima yaliyo mengi, uzalishaji wake uko chini, tija iko chini, ndiyo maana tunaona kuna hasara. Kazi yetu kama Wizara, ni kuhakikisha kwamba tunafanya utafiti wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, labda niliseme hili, wengi wamesema kwa mfano kuhusu mbolea, nami nakubaliana. Wengi wanasema kuhusu pembejeo, lakini kazi ya kwanza ambayo tunatakiwa tuifanye na ambayo sasa tunaifanya, naomba niliambie Bunge lako hili, ni kufanya utafiti wa ardhi yote ya nchi hii ya kilimo ili kuiona ina virutubisho gani? Ina kitu gani kinachokosekana ili tujue aina sahihi ya pembejeo zinazohitajika kwenye lile eneo. Siyo suala la ku-apply tu mbolea, ni suala la lazima kufanyike utafiti.

Mheshimiwa Spika, Kituo chetu cha Mlingano kile cha Tanga karibu kinakamilisha hiyo kazi ya kufanya mapping. Tukishajua hilo, tutajua aina ya mbolea inayotakiwa, tutajua kumbe inawezekana siyo hiyo CAN tunayoisoma au siyo DAP. Lazima tuangalie ni madini gani yanakosekana pale, ndiyo tutengeneze, ndiyo tulete hiyo mbolea.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, mtazamo wa mbolea sasa hivi ndiyo ulioharibu ardhi kwa kiwango kikubwa katika nchi yetu. Sasa hivi wataalam wanasema, inawezekana tukifanya utafiti tutahitaji kuzalisha chokaa ya kutosha ambayo iko nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze, Dodoma kuna kiwanda kinazalisha chokaa. Ile chokaa tungekuwa na uwezo, baada ya kufanya utafiti wa ardhi yetu, tukaenda tukaitumia kwenye mashamba yetu, tusingehitaji kutumia mbolea hata siku moja. Kwa sababu kutumia mbolea maana yake nini? Ukisoma ile mbolea ni sulpher sijui nitrogen; ni madini yaliyokosekana kwenye ardhi.

Mheshimiwa Spika, maana yake nini? Maana yake uchachu (acid) uko juu. Sasa ili kuupunguza uchachu, unahitaji alkaline. Kwa sababu unahitaji alkaline, ile lime ndiyo inaweza ikapunguza hicho kitu chote kikapotea. Kwa kwa mantiki hiyo, inawezekana tusihitaji kabisa hizo mbolea, tutaweka mkazo katika kuhakikisha hiki kiwanda kinazalisha chokaa ya kutosha na tutoe elimu kwa wananchi ili waweze kuanza kujua kutumia chokaa badala ya kufikiria tu kununua mbolea.

Mheshimiwa Spika, nakubaliana kwamba kilimo ndiyo kitatoa mchango mkubwa kwenye viwanda vyetu ambavyo tunasema, nasi kama Serikali tutaendelea kushirikiana kwa pamoja kuhakikisha kwamba viwanda vyetu vinapata malighafi. Sote tunajua, viwanda vyetu vinategemea asilimia 66.5 ya malighafi zinazotokana na kilimo.

Mheshimiwa Spika, kazi yetu sisi sasa Wizara ya Kilimo ni kukaa na wenzetu wa Viwanda ili watuambie ni aina gani ya malighafi wanaihitaji yenye ubora wa kiwango gani kusudi tuhamasishe uzalishaji unaoendana na mahitaji ya soko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na wale wote waliosema kuhusu masoko, siku za nyuma hatukuweka mkazo wa kutosha, hatukuweka msisitizo wa kutosha kwenye upande wa masoko, na hapa ndiyo tatizo. Wananchi wengi walikuwa wanazalisha mazao lakini walikuwa hawajui wapi kwa kuuza. Ndiyo maana kama Wizara kwa kushirikiana na Wizara na taasisi nyingine sasa hivi tumeweka mkazo kwamba lazima suala la masoko lipewe kipaumbele ili kujua masoko ya kila zao yako wapi na wananchi wanapoambiwa kuzalisha basi tuwaambie hili soko liko huku na bei zake ziko hivi. Hiyo tutakuwa tayari tume-link pamoja uzalishaji na masoko yaliyoko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesikitika mdogo wangu Mheshimiwa Haonga anaposema hatujashughulikia mazao, tumeshughulikia mazao yote. Tulipoingia tumesaini mkataba mkubwa wa tani 36,000 ambapo Mheshimiwa Rais wetu ameshuhudia wa kununua mahindi ambapo WFP wamenunua; lile lote ni soko la mahindi. Unaposema kwamba eti hatujashughulikia utakuwa unazungumza vitu vya ajabu. Wizara kila mahali tunatafuta masoko, sasa hivi tumepata soko DRC lakini tumepata vikwazo mahali pa kupitisha kule nchini Zambia ambapo tunaendelea na mazungumzo ili kusudi watu wetu waende kuuza kule nchini Kongo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wamezungumzia Tume ya Ushirika kwamba inawafanya kazi wachache, haina uwezo, nakubali kweli wafanyakazi ni wachache na kazi yetu kubwa ni kuijengea uwezo Tume ya Ushirika ili iweze kufanya kazi iliyokusudiwa kwasababu ndiyo tarajio la wakulima wengi wa nchi hii na ndiyo njia pekee ya kuweza kutatua changamoto zao mbalimbali. Haya matatizo tunayozungumzia kwenye mfumo wa usambazaji wa pembejeo na mambo mengine ni kwa sababu ushirika wetu haujasimama imara. Ni imani yetu tukiusimamisha vizuri haya mambo yatapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo basi, mwaka huu tunategemea kama mambo yataenda kama tulivyopanga tutapata watu 86 ambao tutawaajiri kule kwenye ushirika. Hata hivyo, bado tunaendelea kushauriana na TAMISEMI ili wale wanaushirika walioko chini ya TAMISEMI waweze kuhamishiwa kwetu kusudi waweze kufanya kazi za ushirika.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru lakini kama zitahitajika taarifa zaidi tuko tayari kutoa taarifa ili Bunge lako liweze kujua na takwimu nyingi bado tunazo. Nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuweza kuhitimisha hoja yangu.

Mheshimiwa Spika, kabla ya kutoa maelezo ya hoja mbalimbali zilizoibuliwa na Waheshimiwa Wabunge niwatambue Waheshimiwa wote waliochangia kwa maandishi na kwa kuongea. Hoja hii imechangiwa na jumla ya Waheshimiwa Wabunge 89 wakiwemo Waheshimiwa Wabunge 47 waliochangia kwa kuzungumza humu ndani Bungeni na Waheshimiwa Wabunge 42 waliochangia kwa maandishi. Nitambue kipekee mchango uliotolewa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, nawashukuru sana kwa maoni yao mazuri na mapendekezo yote na ushauri ambao wameshautoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwani wametoa hoja nzuri zenye malengo ya kuimarisha utekelezaji wa majukumu katika Wizara yangu na kuharakisha Mapinduzi ya Kilimo chetu hapa nchini. Hii inaonesha umuhimu wa kilimo katika usalama wa chakula, lishe, ukuaji wa uchumi, na kupunguza umaskini.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Omary Tebweta Mgumba (Mb) na Mheshimiwa Innocent Lugha Bashungwa (Mb) kwa kuchangia hoja hii na kutoa ufafanuzi wa hoja mbalimbali zilizotolewa na Wabunge, nawashukuru pia Katibu Mkuu Mhandisi Methew John Mtigumwe, Naibu Katibu Mkuu Profesa Siza Tumbo, na watendaji wote wa Wizara na Taasisi zake kwa ushirikiano na ushauri wanaoendelea kunipa katika utekelezaji wa majukumu yangu. Michango iliyotolewa ni mingi sana na yote ni muhimu sana. Hata hivyo kutokana na ufinyu wa muda nitafafanua baadhi ya hoja zilizotolewa ambazo ni muhimu Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwa ujumla wakapata ufafanuzi wa moja kwa moja. Ninawahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba majibu ya hoja zote zilizotolewa yataandaliwa na kukabidhiliwa kwa Waheshimiwa Wabunge kabla ya kumalizika kwa mkutano huu wa Bunge la Bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kujibu hoja ya Waheshimiwa Wabunge kwa kueleza mwelekeo wa Serikali katika kuleta mapinduzi ya kilimo hapa nchini. Sote tunatambua umuhimu wa kilimo katika usalama wa chakula, lishe, ukuaji wa uchumi, malighafi za viwandani na kupunguza umaskini. Sote tuko hapa kwa sababu tumepata chakula tumekula, ama kama hatujala muda huu tutakula jioni au usiku; kwa hiyo sisi wote ni wadau katika suala hili.

Mheshimiwa Spika, vilevile Tanzania kama sehemu ya dunia imesaini makubaliano ya kimataifa kuhusu Malengo ya Maendeleo Endelevu, (Sustainable Development Goals – SDG). Chini ya makubaliano hayo ya kimataifa lengo namba moja linahusu kutokemeza umaskini na lengo namba mbili ni kukomesha njaa ifikapo mwaka 2030. Malengo hayo yanamaana kubwa kwenye kilimo kwani kama tunataka kutokomeza umaskini na kukomesha njaa ni lazima tuwekeze kwenye kilimo kwa kufanya mapinduzi yenye kuongeza tija na uzalishaji, kuwa na uhakika wa kuzalisha mazao bora kwa ajili ya malighafi za viwandani na masoko ya ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa Mapinduzi ya Kilimo na kama nilivyowasilisha kupitia hotuba yangu Serikali inatekeleza Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya pili ASDP II. Programu hii inalenga kuleta mageuzi makubwa ya sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi ili kuongeza uzalishaji na tija katika kilimo. Sisi sote ni mashahidi tunaona tija ilivyo ndogo sana katika maeneo mengi kwenye kilimo chetu. Tunakusudia kufanya kilimo kiwe cha kibiashara zaidi na kuongeza Pato la Taifa kwa wakulima wadogo kwa ajili ya kuboresha maisha yao. Pia tunahitaji kuwa na uhakika na usalama wa chakula na lishe na kuchangia katika Pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, historia inatuonesha kuwa nchi nyingi duniani zimepiga hatua kubwa kwa maendeleo kutokana na mchango wa sekta ya kilimo. Nchi kama Uingereza, China, Malaysia, Canada, Korea, Indonesia na nchi nyingine nyingi zimeendelea kwa sababu ya mchango mkubwa wa kilimo katika uchumi wao. Nchi nyingine hizo uchumi wao ulianza kwenye Mapinduzi ya Kilimo na kuelekea kwenye Mapinduzi ya Viwanda. Tunaona kabisa kwa mfano Uingereza ilianza na Agrarian revolution, ambayo ilikuwa ni agricultural revolution ikaja industry revolution na baadaye wakaenda kwenye commercial revolution na political revolution na hatimaye sasa hivi wako kwenye teknolojia ya maendeleo kabisa. Kwa hiyo kwa kweli kila nchi mchango wa kilimo ni mkubwa sana katika hatua ambayo wamefikia.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumeona nchi nyingi sasa hivi zimefikia kwenye ugunduzi mkubwa wa kuboresha, yaani kuwa na huduma nzuri yaani service industry na sasa nyingi zimeingia katika uzalishaji wa teknolojia. Nina uhakika hatuna namna ya kukwepa kama taifa, na ndiyo maana katika hotuba yangu nilibainisha baadhi ya maeneo muhimu yanayohitaji msukumo wa kipekee na maboresho kuanzia mwaka 2019/2020. Maeneo hayo ni pamoja na maboresho ya sera, na Sheria, kuimarisha mifumo ya upatikanaji wa pembejeo za kilimo, masoko ya uhakika ya mazao na bidhaa za kilimo, na kuwakinga wakulima na majanga kupitia Mfumo wa Bima ya Mazao. Ndiyo maana tumeanza mapitio ya sera ya kilimo ya mwaka 2013, mapitio ya sera ya ushirika pia ya mwaka 2002, pia tumeanza mchakato mkubwa wa kuanza mchakato wa kutunga Sheria ya Kilimo na kuandaa utaratibu wa Bima za Mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ili mabadiliko ya kweli ya kilimo yaweze kutokea lazima tuchukue hatua za kusimamia matumizi endelevu ya ardhi kwa kuwa na sera nzuri, na sheria ya kusimamia matumizi ya ardhi ya kilimo, ikiwa ni pamoja na kupima afya ya udongo ili kuwezesha wakulima kuongeza virutubishi vya udongo ardhini kulingana na mahitaji ya udongo. Vilevile matumizi endelevu ya maji ni muhimu sana katika kuongeza uzalishaji na tija ikizingatia mabadiliko makubwa ya tabianchi yanayotokea duniani na nchini kwetu.

Mheshimiwa Spika, mabadiliko ya kweli pia yanahitaji uzalishaji wenye tija na faida katika minyororo ya thamani ya mazao yote; katika eneo hili Serikali imejipanga kuongeza matumizi ya pembejeo bora za kilimo ikiwa ni pamoja na uzalishaji na usambazaji wa mbegu bora za mazao kama vile mahindi, mtama, ngano, ulezi, uwele, maharagwe, na jamii nyingine ya mikundi, alizeti, michikiti, ufuta, karanga, muhogo, parachichi na miwa. Mazao mengine ni kahawa, pamba, pareto, tumbaku, korosho, viazi mviringo, ndizi na zabibu.

Mheshimiwa Spika, tumeanza kuona mabadiliko katika ukuaji wa sekta ya kilimo. Takwimu rasmi za ukuaji wa kilimo zinaonesha kuwa sekta ya kilimo ilikuwa kwa asilimia 6.9 kwa mwaka 2014 na hizi takwimu ni baada ya kubadilisha ile re-base na Kambi Rasmi ya Upinzani ilitoa takwimu namna uchumi ulivyokua, sasa takwimu halisi ambazo ndizo sahihi zinaonesha kuwa kilimo kilikua kwa asilimia 6.9 kwa mwaka 2014, asilimia 5.4 kwa mwaka 2015, asilimia 4.8 kwa mwaka 2016, asilimia 5.9 kwa mwaka 2017 na asilimia 5.3 kwa mwaka 2018. Hizi ndizo official takwimu zinazoonesha ukuaji wa sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, ukuaji huu mzuri wa sekta ya kilimo umetuhakikishia usalama wa chakula nchini kwa muda wa miaka minne iliyopita. Kama nilivyosema kwenye hotuba yangu utoshelevu wa chakula kwa mwaka 2018/2019 ni asilimia 124. Hata hivyo kuna dalili za kutokea upungufu wa chakula katika baadhi ya maeneo kutokana na upungufu wa mvua na mvua kuchelewa katika badhi ya maeneo.

Mheshimiwa Spika, hivyo tuendelee kuhifadhi chakula katika ngazi ya kaya na Serikali kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula itanunua chakula cha kutosha na kuhifadhi kwa ajili ya kukabiliana na upungufu unaoweza kujitokeza. Hata hivyo niwahakikishie wananchi kwamba Serikali haitarajii kuzuia wakulima na wafanyabiashara kuuza mazao yao nje ya nchi, narudia hata hivyo niwahakikishie wananchi kwamba Serikali ya Awamu ya Tano haitarajii kuzuia wakulima na wafanyabiashara kuuza mazao yao nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuongeza matumizi sahihi ya mbolea viuatilifu mbalimbali kama copper, sulfur, na matumizi ya teknolojia za kilimo. Pia tutaboresha matumizi ya dhana za kilimo na kuimarisha huduma za ugani, utafiti na mafunzo. Sanjari na kuongeza uzalishaji suala la masoko ya uhakika wa mazao yanayozalishwa limepewa na litaendelea kupewa kipaumbele kutoka na kuwepo kwa ongezeko la uzalishaji hapa nchini na mahitaji katika masomo ya ndani nje ya nchi. Masoko yataimarika zaidi kwa kujenga viwanda vya kuongeza thamani ya mazao yakiwemo mazao kama kahawa, mahindi, mbaazi, korosho, parachichi, pareto, tumbaku, mkonge matunda na mbogamboga. Aidha, tutaimarisha ukusanyaji wa takwimu za kilimo, huduma za fedha zinazotolewa kama mikopo na vitu vinginevyo, Bima ya Mazao, usafishaji, utunzaji wa mazao na kujenga uwezo wa wataalam wetu katika maeneo mbalimbali ili waweze kutoa huduma zile zinazohitajika kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo ya jumla naomba nitoe ufafanuzi wa maeneo machache kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingi ambazo zimetolewa kama nilivyosema kwamba sitaweza kuzijibu zote zingine tutazijibu kwa maandishi. Hata hivyo naomba nianze na hoja namba moja ambayo ilikuwa imetolewa; kwamba hoja hii inahusu ushuru wa usafirishaji wa korosho ghafi nje ya nchi yaani Export Levy kurudishwa kwa wakulima kwa ajili ya kuendeendeleza zao la korosho. Hoja hii ilichangiwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge, pia Mheshimiwa Cecil Mwambe naye alichangia hoja hiyo.

Mheshimiwa Spika, naomba nikumbushe kwamba Bunge lako Tukufu limeifanyia marekebisho Sheria ya fedha ya mwaka 2018, kifungu cha 17 (a). Kwa mujibu wa marekebisho hayo fedha za ushuru wa usafirishaji wa korosho ghafi nje nchi zitaingia katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Kwa sasa tasnia ya korosho inahudumiwa moja kwa moja na Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, na Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi, tulikaa wote hapa tulipitisha ile kwa pamoja. Kwa hiyo hilo sasa suala hilo tena halipo.

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili iliyotolewa ilikuwa inahusu Serikal iondoe ushuru kwenye Pembejeo za Kilimo kama mbolea, mbegu na viuatilifu. Hoja hiipia ilichangiwa na Mheshimiwa Neema Mgaya, naomba niseme mchango ulikuwa mzuri sana tunaipokea.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya ushuru wa forodha wa Afrika Mashariki (The EAC Costumers Management Act of 2004) na Sheria ya kodi ya ongezeko la thamani VAT Act of 2014, pembejeo za kilimo ikiwemo mbolea, mbegu na viutalifu havitozwi kodi wala ushuru wowote. Naomba nirudie, pembejeo za kilimo ikiwemo mbolea, mbegu na viuatilifu hazitozwi kodi wala ushuru wowote. Aidha, Serikali inaendelea kufanya maboresho ya tozo, ada, ushuru na kodi mbalimbali katika sekta ya kilimo kwa lengo la kuvutia wawekezaji na kuwaongezea wakulima kipato.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi miaka mitatu kuanzia mwaka 2015 Waheshimiwa Wabunge mlifanya kazi nzuri sana katika mjadala, mkasema kuna kodi nyingi sana ambazo ni kero ambazo ni tozo kwenye kilimo mkaiagiza na kuishauri Serikali iziondoe. Nyote mnakumbuka kwamba kuanzia mwaka 2015 jumla ya ushuru tozo na ada 105 zilifutwa kati ya kodi 146 zilizokuwa zinatozwa na kubainika kuwa kikwazo katika maendeleo ya sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa pembejeo Serikali katika mwaka 206/2017 ilifuta jumla ya tozo na ada saba katika tasnia ya mbegu, nne katika tasnia mbolea na moja katika mfuko wa pembejeo. Aidha, Serikali imefanya marekebisho ya kanuni zilizoanzisha tozo na ada hizo kwenye pembejeo ili kuwezesha utekelezaji wake kuwa mwepesi.

Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali imefanya marekebisho ya Kanuni ya Sheria ya Mbolea ya Mwaka 2011 (The Fertilizer Regulation of 2017) ambapo gharama za uhakiki wa ubora wa mbolea imepunguzwa kutoka dola 30,000 hadi kuwa dola 10,000, na muda wa majaribio umepunguzwa kutoka miaka mitatu hadi msimu mmoja katika maeneo mawili ya ikolojia tofauti. Wizara pia ilitunga Kanuni za Kusimamia Ununuzi wa Mbolea kwa Pamoja [Fertilizer Bulk Procurement System (BPS] ambapo imekadiliwa kupunguza bei ya mbolea kwa mtuamiaji wa mwisho kati ya asilimia 10 mpaka asilimia 40 ya bei.

Mheshimiwa Spika, hapa naomba nitoe maelezo kwa undani. Sasa hivi katika utafiti ambao tumeufanya na kuangalia bei ya mbolea nchini na maeneo yote duniani inaonekana kwamba mbolea gharama kubwa ya mbolea inaanzia pale mbolea inapowasili bandarini, kuanzia pale bandarini, gharama za kuitoa pale kuweka kwenye mifuko na kusafirisha mpaka kwa mkulima. Kwa utafiti uliofanyika unaonesha kwamba gharama zile ziko kati ya asilimia 40 mpaka asilimia 60. Kwa hiyo ina maana kwamba tukifanyia kazi vizuri katika hili eneo kuna uwezekano mkubwa mbolea zikashuka bei na zikawa na bei ambayo mkulima anaweza kufaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunakusudia kufanya marekebisho hayo na ndiyo maana tunaupitia upya huu mfumo na hivi kesho tumeita kikao cha wadau wote wanaonunua na kuagiza mbolea nchini wanakuja hapa Dodoma tuna mkutano nao kwa ajili ya kukaa na kujadiliana vizuri kuangalia gharama zote za uendeshaji ili kusudi ikiwezekana mbolea hii ambayo inaagizwa basi ipunguzwe bei na wakulima wetu wapate mbolea ambayo ni sahihi na ile yenye bei nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya tatu ambayo ilikuwa inahusu kuteua Bodi ya Wakurugenzi wa Bodi ya Korosho kwa mujibu wa Sheria. Hoja hii ilichangiwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, pia Mheshimiwa Abdallah Chikota amechangia vizuri sana na wengine waliochangia.

Mheshimiwa Spika, mamlaka ya uteuzi zimeanza uundaji Bodi ya Wakurugenzi wa Bodi ya Korosho Tanzania kwa mujibu wa sheria ya tasnia ya korosho namba 18 ya mwaka 2009 na kanuni za korosho za mwaka 2010. Kazi hii itakamilishwa na Serikali baada ya muda mfupi ujao. Naomba nilitaarifu Bunge lako Tukufu tayari tulishamteua Kaimu Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Korosho ana takriban wiki mbili alisharipoti kazini na wiki hii tunakamilisha uundaji wa Bodi Wajumbe watatangazwa. Kwa hiyo ninauhakika sasa jukumu lile ambalo wanalo lile la kisheria la kuhakikisha wanasimamia zao la korosho wataendelea kusimamia jukumu hilo moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, lakini naomba nitoe angalizo na utofauti uliopo. Kulikuwa na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, bodi ile ilikuwa haisimamii zao, ilienda kama mnunuzi, na kama wanazo fedha wataendelea kununua wakishindana na wafanyabiashara wengine watanunua na kuendelea kuuza. Lakini Bodi ya Korosho itasimamia taratibu zote kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, hoja ya nne ilikuwa ni wadau mbalimbali wa korosho hususani halmashauri bado hawajalipwa fedha na hivyo kushindwa kutekeleza majukumu yao. Hoja hii pia ilichangiwa na Wajumbe wengi na Waheshimiwa Wabunge wengi akiwemo Mhandisi Edwin Ngonyani, pia Mheshimiwa Chikota alichangia na wengine wengi.

Mheshimiwa Spika, Serikali imelipa jumla ya bilioni 26.3 kwa watoa huduma mbalimbali walioko kwenye mnyororo wa thamani wa korosho. Watoa huduma hao ni pamoja na wasafirishaji, AMCOS Vyama Vikuu vya Ushirika, waendesha maghala na gharama za magunia. Kwa kuwa uwamuzi wa Serikali wa kununua korosho kulilenga kumnufaisha mkulima hivyo baadhi ya gharama zimebebwa na Serikali zikiwemo Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninachotaka kusema ni kwamba katika wale wadau ambao bado hawajalipwa sasa hivi tukishapata fedha tutahakikisha kwamba nao basi wanalipwa; lakini lazima tukumbuke kanuni inayoelekeza; Serikali moja haiwezi kuitoza kodi Serikali nyingine. Kwa hiyo ukisema Serikali Kuu ilipe Serikali za Mitaa kidogo kwa mujibu wa kanuni na sheria za kodi ni tofauti. Kwa hiyo hapa tunapozungumzia tunazungumzia wale wadau wengine wote waliotoa huduma ambao si Serikali, hao wote tuna uhakika watalipwa bila tatizo lolote.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa na hoja kwamba wakulima wengi bado wanadai, naomba nikiri kabisa kweli kuna wakulima mpaka sasa hivi hatujamaliza kuwalipa, zaidi ya bilioni 100 za malipo ya korosho bado zinadaiwa, na mimi nakubaliana kabisa na Waheshimiwa Wabunge, wameliongelea suala hili kwa uchungu mkubwa na mimi kama Waziri wa Kilimo linaniumiza sana, nakosa hata usingizi kwa sababu mimi tungependa wakulima wetu wapate fedha kwa wakati ili waendelee kulima; hatutaki kuona wakulima wanahangaika. Kwa hiyo hili kwa kweli sote linatusumbua, lakini tatizo limekuwa ni upatikanaji tu wa fedha za kutosha za kuhakikisha kwamba tunalilipa.

Mheshimiwa Spika, naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali inaendelea kufanya malipo kwa wakulima kulingana na uhakiki uliofanyika; hadi kufikia Mei mwaka 2019 Serikali ilikusanya jumla ya tani 222,830.5 za korosho ghafi zenye thamani ya shilingi bilioni 722, 775,186,000, kati ya hizi fedha jumla ya shilingi bilioni 623,680,510,416 zimelipwa kwa wakulima moja kwa moja ambayo hii ni sawa na asilimia 86 ya madai yote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa kweli Serikali tumejitahidi hatukutegemea kwanza halikuwa lengo kwamba zile fedha labda tutachelewa, tulidhani kwamba baada ya kukusanya tukiuza, tungezungusha zile fedha wakulima wote wangekuwa wamelipwa. Mpaka sasa hivi hatujauza lakini Serikali imelipa zaidi ya bilioni 623, tumejitahidi. Hii haina maana kwamba tunabeza wale ambao hawajalipwa kwa sababu moja ya watu ambao hawajalipwa ni wale wakulima wakubwa ambao mimi nataka walipwe ili waendelee kulima zaidi na kuhudumia kilimo. Kwa hiyo hili tutaendelea kulifanyia kazi na kwa muda mfupi nina uhakika Serikali tutaliangalia na kuhakikisha kwamba tunapata fedha kwingine hata kwa kukopa ili wakulima hawa walime waendelee kupalilia korosho zao na waendelee kuzalisha, kwa hiyo hili tutaendelea kulishughulikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingine kwamba tujikite kwenye ubanguaji, wawekezaji kwenye viwanda vya Serikali walioshindwa kuviendeleza wanyang’anywe. Nakubaliana kabisa na maoni ya Waheshimiwa Wabunge, nchi yetu ni kubwa wala hatuwezi kulinganisha na nchi nyingi, ni nchi iliyobahatika kuwa na ardhi nzuri yenye uwezo mkubwa, yenye watu wengi wenye utaalam mkubwa. Sasa hivi Msumbiji wanabangua korosho zao kwa asilimia 75, sisi nchi kubwa yenye wataalam wengi, korosho zetu zote tunauza zikiwa ghafi. Hii haikubaliki na ndio maana hata viwanda tulivyokuwa navyo vyote, Mheshimiwa Baba wa Taifa marehemu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alianzisha viwanda 12, tukavibinafsisha, tukawauzia watu, baadhi ya watu waliochukua wameshindwa kuviendeleza wala havifanyi ile kazi, ndio maana kwa sababu hiyo Serikali tumeamua kuvirudisha baadhi ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe takwimu, viwanda vinne sasa hivi tumeshavirudisha mikononi mwa Serikali ili kusudi tuwekeze, viendelee na kazi ya kubangua, kusudi korosho zetu zote zibanguliwe hapa nchini. Kwa hiyo tumechukua Kiwanda cha Kubangua Korosho cha Lindi kile cha Buko, wote mnajua. Pia tumechukua kiwanda cha Newala yaani Agrow Focus nacho tumekitaifisha, tumeshakirudisha, tumemnyang’anya yule mwekezaji. Vile vile Kiwanda cha Mtama yaani kile cha Lindi Farmers tumekichukua, Kiwanda cha Nachingwea nacho tumekichukua. Kwa hiyo, viwanda vyote hivi tumeshavirudisha, sasa hivi tunatafuta wawekezaji wapya ili wawekeze na wahakikishe kwamba kwa kweli hivi viwanda vinabangua.

Mheshimiwa Spika, najua kulikuwa na tatizo kubwa ambalo walikuwa wanalisema, walikuwa wanasema wanashindwa kushindana kwenye soko kwa sababu wanakosa malighafi, lakini nataka nilihakikishie Bunge tumejipanga vizuri kuangalia upya sera yetu ya uuzaji ili kusudi viwanda vyote vitakavyoanzishwa vihakikishiwe kupatiwa malighafi ili vitoe ajira na kuongeza thamani. Kwa hiyo, hiyo sera itakuwa nzuri sana.

Aidha, Serikali itaendelea kuhamasisha wawekezaji wanye viwanda vya kubangua korosho ili kuongeza uwezo wa ndani wa ubanguaji na kukuza ajira. Serikali itaendelea kutafuta wanunuzi wa korosho zilizohifadhiwa kwenye maghala ili kutoa nafasi ya kuhifadhi korosho kwa msimu ujao. Nitumie fursa hii kuwaomba hata Waheshimiwa Wabunge, wanaweza wakaunda SACCOS ya kwao wakaanzisha viwanda, hebu tuongoze kwa vitendo, tunaweza tukaanzisha viwanda viwili, vitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna viwanda pale vya kubangua korosho unaweza ukaanzisha kwa Sh.1,000,000,000. Nina uhakika kabisa Waheshimiwa Wabunge tulioko hapa haviwezi kutushinda, kinachohitajika ni dhamira ya kweli ya sisi wenyewe kwamba tunataka kweli tujenge viwanda, tunaweza, hili linawezekana, ukilinganisha na mikopo ambayo huwa tunakopa. Tukiwekeza nina uhakika nchi hii itasogea mbele na tutasogea sana.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja kuhusu mawakala ambao hawajalipwa wale ambao walisambaza pembejeo mwaka 2015/2016. Nakubaliana kabisa kwamba kulikuwa na mawakala wengi lakini tulipofanya utafiti, tulipofanya uchunguzi imebainika karibu kila wakala alidanganya, mawakala wote walidanganya. Sasa kama wamedanganya, takwimu ni feki unamlipaje?

Kwa hiyo, sisi tulichokifanya sasa hivi katika hili suala tulipoona kwamba wote kila mtu ana udanganyifu, tumechukua takwimu zao zote tumepeleka TAKUKURU, wanaendelea na uchunguzi, ukikamilika wale watakaobainika kwa kweli hawakudanganya hao wote tutawalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja Serikali kupelekea pembejeo kwa wakulima kwa wakati, bei nafuu na kuweka mfumo mzuri wa upatikanaji wake. Hoja hiii imechangiwa na Wabunge mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji. Pia Mheshimiwa Ngalawa, Mheshimiwa Semesi, Mheshimiwa Kakoso na wengine wengi wamechangia hii hoja. Wizara inakamilisha mapitio wa mifumo ya uzalishaji, uagizaji na usambazaji wa pembejeo ili kuandaa mfumo madhubuti utakaohakikisha kwamba pembejeo zilizozalishwa au kuagizwa nje zina ubora na zinapatikana kwa wakati na kwa bei nafuu kwa mkulima. Aidha, Serikali itahamasisha na kusimamia usambazaji wa pembejeo kwa kuzingatia kalenda ya kilimo katika maeneo mbalimbali nchini kulingana na kanda za kiikolojia za kilimo ili pembejeo zifike kwa wakati unaostahili.

Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali imeliagiza Shirika la Reli Tanzania (TRC) kutoa kipaumbele cha kusafirisha mbolea kwenda mikoa yenye miundombinu ya reli kwa kuwa gharama za usafirishaji kwa njia ya reli ni nafuu ikilinganishwa na usafiri wa barabara. Hili mpaka kuanzia bandarini pale, bandarini pia tumeongea na wenzetu wa bandari kwamba watoe kipaumbele mbolea zinapowasili ziweze mara moja kupakuliwa na kupelekwa katika maghala na ziweze kusafirishwa ziende kule zinakohitajika. Tunajua misimu inatofautiana, kwa hiyo, tumetoa hicho kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa na suala linahusu bajeti ya kilimo kwa kuzingatia Maazimio ya Malabo na Maputo. Hoja hii imechangiwa sana na Kamati ya Kudumu ya Bunge na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imelisema na Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema kwamba bajeti ya kilimo ni ndogo. Naomba nitoe ufafanuzi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kusema bajeti tu haitoshi, ni kweli haitoshi na hakuna siku ambayo tutasema bajeti inatosha, lakini upangaji wa bajeti na vipaumbele unategemeana na nchi moja na nchi nyingine, lakini tunazingatia majukumu ya Serikali ni nini katika hiyo. Kwa mfano katika nchi yetu, Serikali haiendi kulima mashamba, Serikali kazi yake ni kutengeneza miundombinu ili sekta binafsi zikalime, wakawekeza, wakafanye biashara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunachosema sisi ni kwamba, Serikali ndio unaweza ukaiangalia bajeti ya kilimo lakini kitaalam zaidi bajeti ya kilimo haipimwi kwa hela zilizowekwa kwenye Wizara ya Kilimo peke yake, fedha zote ambazo ziko TAMISEMI kwa asilimia kubwa zile ambazo ziko TARURA zote zinatengeneza barabara zinazohudumia kilimo. Fedha zilizoko Wizara ya Uvuvi, fedha zilizoko kwenye Wizara mbalimbali, kwa mfano sasa hivi Wizara ya Nishati wanasambaza umeme vijijini, ule umeme ni kwa ajili ya kuhudumia wakulima. Kwa hiyo yote hiyo tunaita ni bajeti ya kilimo. Barabara mbalimbali zinajengwa barabara kubwa, reli zinajengwa, viwanja vya ndege vinajengwa, vyote hivyo ni kwa ajili ya kuhudumia wakulima. Kwa hiyo ukitaka upate bajeti ya kilimo peke yake ni vigumu, zote hizo zichukue, angalia, sasa ndio unaweza ukakokotoa ukapata bajeti ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema ni kwamba hatuwezi kusema tunaweza kutekeleza hiyo kama ilivyo lakini lazima tuiangalie kwa vipaumbele ambavyo tunatekeleza na nina imani bajeti zilizotengwa kwenye Miundombinu, Nishati, Mawasiliano, Uvuvi, TAMISEMI zote ni kwa ajili ya kuhudumia kilimo chetu na hivyo nina uhakika kabisa kwamba bajeti ni kubwa na itatosheleza katika kutekeleza majukumu ya mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, aidha, Wizara na Taasisi mbalimbali kama vile Viwanda, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Maji, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Wizara ya Ardhi, Wizara ya Ujenzi, Wizara ya Nishati zinachangia katika utekelezaji na ukuaji wa Sekta ya Kilimo. Kwa mfano Wizara ya Ardhi, ardhi yote hii ikipimwa na tunasema kwamba ikipimwa ikaeleweka ardhi ya kilimo ni hii tayari watakuwa wamechangia na itakuwa ni bajeti ya kilimo. Pia kuna ASDP II inatekelezwa na Wizara za Kisekta ikiwepo Wizara ya Kilimo, lakini kuna Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Maji, TAMISEMI, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Uwekezaji na kadhalika. Zote hizo ukiangalia shughuli zao kwa asilimia karibu 80% zote zinashughulikia masuala ya kilimo. Kwa hiyo kilimo, nasema ni suala mtambuka na hivyo bajeti yake bado ni kubwa na inatosheleza.

Mheshimiwa Spika, wapo Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia kuhusu masoko na wamezungumza kwa undani sana. Hoja hii ilichangiwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mifugo na Maji, Kambi Rasmi ya Upinzani walisema, lakini pia baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walichangia sana kuhusiana na masoko. Serikali inaendelea kutafuta masoko ya uhakika ya mazao mbalimbali ndani na nje ya nchi. Kwa kuanzia tumeanzisha Kitengo cha Masoko katika Wizara ya Kilimo ambacho hakikuwepo ili kihakikishe kwamba kwa kweli kinafanya market intelligence, kitafute masoko nje, kitafute masoko ndani na hata ndani hapa masoko bado ni makubwa bado hatujayatumia vizuri. Kwa hiyo, kwa kupitia kitengo hiki ni imani yangu kwamba tutajitahidi sana kuhakikisha hili tunalifanya.

Mheshimiwa Spika, hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kutangaza fursa za masoko ya wakulima, kuingia mikataba ya kibiashara baina ya Tanzania na nchi mbalimbali na kuunganisha wakulima moja kwa moja na wanunuzi kama nitakavyowaeleza hapo baadaye. Aidha, Wizara ya Kilimo inaendelea kutoa vibali vya kuuza na kusafirisha mazao nje ya nchi. Kwa mfano, kati ya mwezi Januari, 2019 na Aprili, 2019; jumla ya tani 22,201 za mbaazi zimesafirishwa kwenda nchi za Qatar, Dubai, Oman, Pakistan, Bangladesh, Malaysia, Kuwait, Indonesia, United Emirates Republic na Ureno. Aidha, katika kipindi hicho jumla ya tani 80,648 za mahindi ziliuzwa nchi za Rwanda, Uganda, Congo, Kenya, Burundi, Malawi, Oman, Sudan ya Kusini na kadhalika na vilevile makampuni yaliyosajiliwa yamenunua mhogo mkavu kati ya tani 254.52 kwa ajili ya kusafirisha kwenda nchini China na kuna kampuni kama tano ambazo zimeshapata vibali vya kusafirisha mhogo.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninachotaka kuwaambia Waheshimiwa Wabunge ni kwamba, hizi jitihada tuendelee nazo. Tutaendelee kuzungumza na nchi mbalimbali, tutaendelea kutafuta wanunuzi mbalimbali wa mazao yetu yote, yale ambayo tunayo na yale mengine tunayoweza kuanzisha ili kuhakikisha kwamba kilimo kinachangia kwa kiwango kikubwa katika uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Serikali ifanye tafiti kwa zao la parachichi kuendana na hali halisi ya mabadiliko ya teknolojia. Nakubaliana kabisa na hoja hizi zilizotolewa na Mheshimiwa Peter Msigwa, Mheshimiwa Neema Mgaya wamechangia kweli, lakini Serikali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) inafanya utafiti wa kuzalisha mbegu pamoja na miche bora ya parachichi na kuisambaza kwa wakulima. Vilevile Serikali imepeleka taarifa muhimu za kisayansi zinazohitajika kwa ajili ya masoko ya parachichi katika nchi ya China na nchi za Ulaya. Taarifa hizo zimefungua majadiliano kwa lengo la kuweka makubaliano ya kibiashara baina ya Tanzania na nchi hizo. Ni imani yetu kwamba tukishaweka makubaliano yatasaidia sana katika kuhakikisha kwamba kilimo chetu kinakwenda mbele na tunapata masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulitolewa hoja nyingine kwamba kipaumbele kitolewe kupeleka fedha katika Vyuo vya Mafunzo na Taasisi za Utafiti. Hoja hii imechangiwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge. Serikali imekuwa ikiongeza fedha kwa ajili ya utafiti mwaka hadi mwaka na hilo ndio lengo letu kwa sababu utafiti ndio uhai wa kilimo, bila utafiti hakuna kilimo. Katika mwaka 2018/2019, jumla ya Sh.697,905,309 zilitengwa kwa ajili ya ukarabati wa maabara za kibaiolojia na bioteknolojia za TARI Tengeru ambapo ilitengewa Sh.399,999,630 na maabara ya kusindika mvinyo ya TARI Makutupora ambayo ilitengewa Sh.297,906,300 kupitia COSTECH. Katika mwaka wa fedha 2019/2020, Wizara imetenga Sh.9,224,033,150 katika bajeti ya fedha ya maendeleo na matumizi ya kawaida. Aidha, TARI Naliendele imetengewa Sh.5,610,547,100 kwa ajili ya kuimarisha na kuendeleza utafiti wa zao la korosho.

Mheshimiwa Spika, zipo hoja nyingi ambazo zimetolewa, lakini kulikuwa na hoja kuhusu utafiti wa udongo na kwamba Serikali ikamilishe kwa haraka. Naomba nilitarifu Bunge lako Tukufu na hoja hii imechangiwa na watu wengi sana. Tathmini ya udongo hadi sasa imefanyika katika mikoa 16 kati ya 26 ya Tanzania Bara na baadhi ya ramani zimeshatolewa kwa vipimo vya aina mbalimbali. Tumeshamaliza katika kanda zote kama nilivyoahidi kwenye Bunge la mwezi wa Pili kwamba tunafanya tathmini katika kanda zetu zote kuweza kubaini udongo uliopo na kuangalia virutubishi ambavyo vinakosekana katika ule udongo.

Mheshimiwa Spika, naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba kazi hii imekamilika na tayari tunayo ramani inayoonesha nchi nzima, ninazo hapa ramani zinaonesha ni aina gani, udongo wetu una nini, vitu gani vinakosekana, vipo hapa na ramani kubwa tunazo tumeziacha pale chini. Ramani zimekamilika, kwa hiyo tuna uhakika, hii kazi imekamilika lakini tunaendelea sasa kwenda mkoa kwa mkoa ili tukipata mkoa kwa mkoa tutajua mkoa huu unahitaji nini na kinakosekana nini.

Mheshimiwa Spika, lengo la hii yote ni nini? Lengo hasa ni kutaka kujua kwamba wanapotumia mbolea tuweze kuwaambia mbolea ambazo ni sahihi kulingana na mahitaji ya udongo na wakati mwingine watu wananunua mbolea unakuta kwamba labda hiyo mbolea vile virutubisho vilivyopo mle ndani havihitajiki. Kwa hiyo ndio maana tumeamua kwamba kuanzia mwaka huu tunafanya jitihada na wawekezaji ili wajenge kiwanda cha kuchanganyia mbolea. Baada ya utafiti huu tuwe na kiwanda sasa ambacho tumekubaliana kinajengwa pale Dar es Salaam, tunatumia magodauni ya pale Dar es Salaam kichanganywe mbolea yaani ile blending plant, tunaweka mwaka huu, ili kusudi wakulima wakisema mahitaji ya udongo wangu yako hivi, basi tunajua mbolea anayohitaji inatakiwa hii na hii. Nina imani kama hilo litafanyika tutaendelea vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja kuhus uzalishaji wa mbegu za mafuta, lakini pia uzalishaji wa mbegu hapa nchini bado hautoshelezi. Nakiri kabisa kwamba tuna changamoto kubwa kwenye uzalishaji wa mbegu tunazozihitaji na mpaka sasa hivi uwezo wa nchi kuzalisha mbegu ni karibu asilimia 64 tu ya mahitaji yote, lakini tumeamua kuweka jitihada na kuweka mikakati ya kutosha kuhakikisha kwamba tunapata mbegu zile ambazo tunazihitaji. Kwa hiyo Serikali imeamua kuwekeza vya kutosha katika uzalishaji wa mbegu za mafuta ili kujitosheleza kwa mafuta ya kura na ziada kuuza nje.

Mheshimiwa Spika, kwa kuanzia Wizara imeanza mkakati wa kundeleza zao la mchikichi unaolenga kuzalisha mbegu bora za michikichi kwa kipindi cha miaka minne kuanzia mwaka 2018/2019 mpaka 2021/2022. Katika mwaka 2019/2020, Wizara kwa kushirikiana na wadau wengine wakiwemo JKT na Magereza itazalishwa miche ya michikichi 5,000,000 kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa zao hilo. Mkakati huu unatekelezwa sambamba na kuwapatia wakulima teknolojia bora za kuongeza thamani kupitia SIDO, TADB, CAMARTEC, NDC na UNIDO.

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kabisa kwamba kwa kweli tunahitaji mbegu zilizo bora na kama nchi lazima tuwekeze kwenye mbegu zilizo bora. Hili tuna imani kabisa tutalifanyia kazi vizuri na nitumie fursa hii kuziomba taasisi zingine hapa tumesema JKT na Magereza lakini nina uhakika taasisi zingine zinaweza zikawekeza kwenye uzalishaji wa mbegu, taasisi binafsi, taasisi za umma hasa wanawekeza lakini bado haitoshi.

Mheshimiwa Spika, kwa nini tunahitaji mbegu za kutosha kwa upande wa michikichi? Nchi ya Malaysia ambayo miaka ya nyuma ilichukua mbegu za michikichi kutoka Tanzania inazalisha mafuta, inazalisha mafuta yanayotokana na michikichi kwa wingi sana duniani, lakini mbegu zilitoka kwetu. Sisi wenye ardhi nzuri na ambao tulitoa mbegu, uzalishaji wetu uko chini. Sasa hivi tunatumia zaidi ya bilioni 674 kwa mwaka kuagiza mafuta ya kula, wakati uwezo wa kuzalisha hapa nchini upo, tuna uwezo wa kulima alizeti kwa wingi, tuna uwezo wa kulima michikichi kwa wingi, tuna uwezo wa kulima karanga, tuna uwezo wa kulima mbegu za pamba na nyinginezo, tukazalisha mafuta ya kutosheleza nchi yetu. Kwa nini kila wakati tuagize au tutumie fedha zetu kuagiza nchi za nje wakati sisi tuna uwezo wakuzalisha? Hili ni lazima tulivalie njuga na nitaomba ushirikiano wa Waheshimiwa Wabunge wote tuhakikishe kwa kweli hili tunalisimamia kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia pamoja na uzalishaji wa miche ya michickichi Serikali kupitia TARI inakamilisha utafiti wa mbegu mpya za alizeti zenye uwezo wa kutoa mavuno na mafuta mengi, ili kuhakikisha wakulima wanapata mbegu bora kwa gharama nafuu badala ya kuagiza kutoka nchi za nje. Bahati nzuri nimepata maombi mengi kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge, wananiuliza na wananiomba mbegu bora, wengine wameomba za michikichi, na wengine wameomba za alizeti.

Mheshimiwa Spika, na mimi niseme tu nitahakikisha wote mnapata hizo mbegu, ili kusudi mwende kulima kwa sababu najua ninyi Waheshimiwa Wabunge ndio wadau wangu wakubwa wa kilimo; na ninyi mkilima ndiyo itakuwa mfano hata kwa wakulima kuja kuiga na kuona namna mnavyolima. Maana nchi hii tumefikia mahali unakuta mtu ana ardhi pale hata kupanda miche miwili ya nyanya pale nyumbani hapandi, halafu tunaagiza ilhali ardhi nzuri na kila kitu tunacho. Hii neeme tuliyopewa na Mungu lazima tuitumie vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo hoja ambazo wajumbe wamechangia. Suala la umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, wamezungumzia sana suala la umwagiliaji; na mimi niungane na ufafanuzi mzuri sana alioutoa Naibu Waziri. Nataka niwaambie, katika skimu tulizonazo zote zilizokuwa chini ya umwagiliaji ziko zaidi ya 2,600. Huwezi kupata skimu 10 za mfano zinazofanya kazi, kwa hiyo skimu zote zina matatizo; na sisi tumeangalia ule Muundo wa Tume ya Umwagiliaji tukaona hapa lazima tuifumue. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeshaifumua ndiyo maana tumeanza, sasa tunasema wiki hii tunakamilisha muundo mzima na uongozi mpya, na tunawagawia maeneo ya kusimamia. Tunataka kwenye kanda abaki mmoja kwa sababu kwenye kanda hakuna kilimo. Kwenye mkoa wanakuwa wawili, lakini tunataka wale wote, Maafisa Umwagiliaji, ma-engineer wa umwagiliaji waende kwenye halmashauri zetu zinazoshughulika na kilimo wakasimamie skimu kule chini na kila mtu atawekewa malengo ya kuhakikisha kwamba anasimamia. Mimi nina uhakika tukilisimamia vizuri hili litaweza kutatua tatizo letu la miradi mbalimbali ya umwagiliaji ambayo ilikuwa haifanyi vizuri katika nchi yetu, kwa hiyo hili tumeliwekea mkakati wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ipo hoja ambayo Waheshimiwa wajumbe pia, wamezungumzia. Wamezungumzia suala la kahawa; na mimi ni mdau wa kahawa, naijua kahawa kwa sababu nimekulia kahawa. Nimefurahi sana mlivyoichangia kahawa, nimeona Mheshimiwa Selasini na Waheshimiwa Wabunge wengi wameichangia sana kahawa.

Mheshimiwa Spika, kahawa lilikuwa ni zao la mfano, lilikuwa linatoa mchango mkubwa sana kwa fedha za kigeni miaka ya nyuma, lakini sasahivi limeshuka uzalishaji, tunazalisha takribani tani elfu 50, sasa hivi tumesema tumezalisha tani elfu 64, lengo tunataka tuzalishe tani elfu 80, hazitoshi. Tumeweka mkakati kwenye uzalishaji, wenzetu wa TACRI wakishirikiana na Bodi ya Kahawa tumeamua kuanzisha uzalishaji wa miche ya kisasa, ili kuisambaza kwa wakulima mbalimbali na hili tutalisiamamia ili tupate miche iliyo bora ambayo itaongeza uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, kuna tatizo la bei, wengi wamezungumzia bei, na mimi nimeona kuna tatizo la bei. Mwaka huu nilipoongea na wazalishaji wanasema tunaweza tukapata kahawa safi tani 50,000, pure coffee; nimewauliza wanunuzi wanne wakubwa duniani watuambie wanahitaji tani ngapi? Wanahitaji tani 65,000. Kwa hiyo, ina maana mahitaji ni makubwa kuliko tulichozalisha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tukasema kama hiyo ndio hali basi tuunde kamati maalum ndani ya Wizara, lakini Wizara inatoa mmoja iwe ni kamati huru, tumechukua Benki Kuu, Wizara ya Fedha na taasisi mbalimbali; tumeunda kamati ili ikutane na wanunuzi wakubwa hawa wajadiliane juu ya bei; wakikubaliana iwe ni kazi ya kuuza tu si tena mara kwenye mnada mara nini na nini. Sisi kwenye mnada tunataka twende tupeleke zile zitakazokuwa zimebaki ambazo zitakua hazijanunuliwa ndio maana Naibu Waziri amesema tunasisitiza direct selling, uuzaji wa moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, Dunia nzima nchi nyingi zimeenda katika mikataba ya moja kwa moja, Rwanda wamefunga mkataba na Ujerumani wa miaka kadhaa, na sisi lazima tufike mahali tusaini mikataba ya mauziano ya muda mrefu, hapo ndipo tutapata ufumbuzi wa changamoto zinazoikabili bei. Si kila mwaka eti tutegemee soko watu wa-bid pale, wakiingia kwenye collussion bei inakuwa ndogo wakulima hawafaidiki na sisi utaalamu wetu wengine ni mdogo. Kwa hiyo tunafikiri hii timu itafanya kazi vizuri na nina uhakika baada ya wiki mbili watakuwa wamemaliza. Kwa hiyo, katika msimu huu tutatumia njia ya mauzo ya moja kwa moja na zile zitakazobaki ndizo tutazipaleka kwenye minada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ya pili kwenye minada hii, minada ya kahawa, tulichokubaliana tunafanya kwenye kanda. Kanda ya Ziwa utafanyika mnada kule Kagera, Kanda ya Kaskazini watafanyia Moshi, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Mbeya, Rukwa, Songwe watafanyia Songwe, na Ruvuma pia kutakuwa na Kanda, tutakuwa na kana nne ambazo minada itafanyika. Lengo ni kupunguza gharama kwa ananchi za kuhangaika kwenda kupeleka kahawa yao kule Moshi kwa ajili ya kwenda kuuza kwa hiyo; sasa wanunuzi watakwenda kule kwa hiyo, tuna imani itasaidia kupunguza changamoto zinazotokana na zao la kahawa.

Mheshimiwa Spika, lakini kuna pareto, mmezungumza sasahivi zao la pareto ndio nchi pekee inayozalisha. Pamoja na kwamba, tunazalisha kidogo, lakini ndio nchi pekee. Takwimu zimetolewa za bei za pareto, lakini hazikuwa sahihi sana.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema mimi ni kwamba pareto hii ndiyo tunayotaka tuitumie katika uwekezaji wa kuanzisha viwanda vya viuatilifu. Viuatilifu ili vianzishwe vitatumia pareto yetu. Kwa hiyo mimi nina imani hizi jitihada zitasaidia na zitazaa matunda; lakini pia tunahitaji anunuzi wengine. Sasa hivi kuna mnunuzi mmoja, mnunuzi mmoja atashindana na nani? Lazima kuwe na ushindani ndio tunaweza kupata bei nzuri. Kwa hiyo hili tutalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la mkonge. Miaka ya nyuma Tanzania ilikuwa inaongoza kuuza mkonge nchi za nje, tuliongoza kwa uzalishaji. Sasa hivi tumeshuka tunazalisha kidogo sana. Tumeamua kurudisha heshima ya nchi yetu kuhakikisha tunazalisha mkonge iwezekanavyo. Mashamba ya mkonge yote lazima yafufuliwe na mengine mapya yaanzishwe na changamoto zote tuondokanenazo. Imekuwa ni aibu tunatumia fedha nyingi kuagiza magunia nchi za nje, tunayaleta hapa ilhali tuna uwezo hata wa kutengeneza magunia ya kwetu, lakini pia mahitaji ya mkonge duniani bado ni makubwa. Kwa hiyo tunafikiri nchi yetu lazima irudi kwenye mstari.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kidogo kuhusu zao la tumbaku. Najua muda hautatosha. Tumbaku ina changamoto nyingi na kuna baadhi ya wanunuzi wako wanne tu wakubwa. Mmoja ametoa tishio kwamba, anakusudia kujiondoa mwakani, hajaingia kwenye mkataba. Najua wananchi wanaolima zao la tumbaku wamepata mfadhaiko kidogo. Hata hivyo nataka niwahakikishie kwamba Serikali yenu inafanya majadiliano na huyu mnunuzi, lakini pia tunatafuta wanunuzi wengine. Sasa hivi tumekwenda China tunafanya majadiliano. Tumewaalika waje kuangalia, lakini pia wao wanasema wana mbegu wanazozitaka. Tunataka watuletee hizo zifanyie majaribio waanze kulima. Pia tunaangalia nchi nyingine zinazohitaji hiyo tumbaku. Kwa hiyo pamoja na mambo mengine mimi nina imani mikakati tuliyoiweka itasaidia sana kutatua hili tatizo.

Mheshimiwa Spika, kuna hoja imetolewa kuhusiana na Maafisa Ugani. Maafisa Ugani kweli ni changamoto na mahitaji ni makubwa. Maafisa Ugani kwa mujibu wa muundo wetu wa Serikali wako chini ya TAMISEMI, wale ndio wanasimamia kilimo kule. Sisi kama Wizara ya Kilimo tunatengeneza Sera, tunatengeneza taratibu na miongozo ya kilimo, lakini wanaoenda kusimamia ni wale. Hata hivyo kuna vijiji havina, lakini hata vijiji vingine vina Maafisa Ugani ambako Maafisa Ugani wengine wanakaa bila kufanya kazi. Kwa hiyo sasa hivi kama Serikali tunakaa pamoja na TAMISEMI tunakuja na utaratibu mpya wa kuwasainisha mikataba ya namna ya kusimamia kilimo katika maeneo ambayo wanayasimamia. Kuhusu hoja kuongeza Maafisa Ugani hii tunakubaliananayo tutaendelea kuifanyia kazi kadiri bajeti itakavyoruhusu tutaweza kuendelea kuajiri hao wakulima.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala moja la msingi. Tumeanzisha usajili wa wakulima. Lengo la usajili wa wakulima ni nini?

Mheshimiwa Spika, kwanza kama nilivyosema wakati nawasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara, tumeanza zoezi la usajili wa wakulima wote nchini. Lengo la zoezi hili ni kutaka kutambua walipo, wanalima nini? Wana maeneo yenye ukubwa kiasi gani? Wanahitaji pembejeo za namna gani? Wanahitaji zana gani? Wanahitaji msaada gani? Tukiwatambua hawa wakulima ndio tutaweza kuwahudumia; unamhudumiaje mtu ambaye hujui? Tunataka kila zao tujue kuna wakulima wangapi? Wanalima eneo kiasi gani? Kwa hiyo, hayo ndio tumeyaanzisha.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe taarifa; na kuna mmoja hapa amesema takwimu hazieleweki, nini na nini; naomba niseme, mpaka sasa hivi mazao ya kipaumble ambayo tayari tueshasajili, tumesajili wakulima 1,669,699, hao ndio tunaotegemea kuwasajili. Tuliowasajili ni 1,464,827 ambao ni asilimia 87.3 katika mazao nane ya msingi, yaani kahawa, chai, kosroho, miwa, tumbaku, na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema awali kwamba mambo yote mengine tutawajibu Waheshimiwa Wabunge, hoja najua ni nyingi, lakini nitumie fursa hii, nawashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kutoa ufafanuzi wa baadhi ya maeneo machache kuhusu hoja hii ya Wizara ya Kilimo. Baada ya kusema hayo niwaombe Wabunge kwa heshima kubwa kabisa mkiwa wadau wa chakula, mkiwa wadau wa kilimo, wote kwa pamoja muipitishe bajeti yangu bila matatizo.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipatia hii nafasi ili niweze kuchangia katika wizara hii. Jambo la kwanza, kwanza nawapongeza sana, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Manaibu Mawaziri lakini pia Katibu Mkuu na Manaibu Makatibu Wakuu, Wakurugenzi wote kwa namna ambavyo wamekuwa wanaisimamia hii wizara na wanatekeleza majukumu yao. Hii ni moja ya wizara kubwa ambayo inagusa Maisha ya watanzania kila mahali. Kwa hiyo ni wizara ngumu lakini naamini mungu atakuwa pamoja na nyinyi ili muweze kufanikiwa na kufikia matarajio ya watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, naomba nishauri kwasababu ya ukubwa wa hii wizara na kwa umuhimu wa Wizara ya TAMISEMI ni muhimu tufike mahali tuingie kwenye mikataba ya utendaji. Mikataba ya utendaji itatusaidia kwamba kila halmashauri sasa, halmashauri iangalie mapato ndani, iweke kipaumbele angalau kimoja au viwili kama ni kujenga kituo cha afya mwaka huu wanajenga kituo cha afya, kama ni kujenga ni shule wanajenga shule. Katika halmashauri zote hizo baada ya miaka mitano tutakuwa tumefika mbali sana. Kwa hiyo, nafikiri hili ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu, TARURA, TARURA ni muhimu sana, TARURA ndiyo imebeba barabara mbalimbali zilizopo mijini na vijijini. Kwenye Jimbo langu la Vwawa wananchi wa Jimbo la Vwawa ni wakulima, wakulima wa kahawa, wakulima wa mahindi wa mazao ya chakula na biashara na wanazalisha kweli kweli na ndio maana Mkoa wa Songwe Kitaifa unashika nafasi ya tatu kwenye uzalishaji wa chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ili waweze kuendelea kuzalisha na huduma mbalimbali ziweze kuwafikia wakulima tunahitaji barabara zao ziimarishwe, zifike mpaka vijijini kule ili wale wananchi sasa waweze kupata pembejeo kwa wakati waweze kusafirisha mazao yao kwa muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika kufanya hilo barabara kama ile barabara ya kutoka Iyula kwenda Idunda kwa muda mrefu imekuwa haipitiki. Wananchi wale wa Idunda kwasababu ya mvua nyingi daraja lilikatika barabara haipitiki wanakosa huduma mbalimbali naomba barabara hii iyangaliwe. Kuna barabara ya kutoka Ichenjezya kwenda Mbozi Mission. Kuna barabara ya kutoka Ichenjezya kwenda Msia hizi barabara ni muhimu sana kwasababu zinaenda katika maeneo ya uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna barabara ya kutoka Chimbuya, Ukwile kwenda Chizumbi pale kuna daraja kubwa lilikatika wananchi wale wanakuwa hawana mawasiliano kipindi cha mvua ni muhimu TARURA wakaongezewa fedha ili waweze kujenga haya madaraja, wajenge barabara hizi zipitike kwa wakati wote na tunaamini uzalishaji utakwenda vizuri sana katika hali kama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara nyingine ambayo inatoka njiapanda ya Iyula inaenda mpaka Iyula, ile barabara ni muhimu sana, sasa hivi imeharibika kabisa, utakuta kwamba wanashindwa kupeleka mbolea, wanashindwa kusafirisha kahawa, wanashindwa kupata huduma mbalimbali naomba hili nalo liangaliwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara nyingine ya kutoka Ihanda inaenda mpaka Ipunga pamoja na kwamba imekarabatiwa bado kuna mambo hayajakaa vizuri katika eneo hilo. Kwa hiyo, ushauri wangu ni vizuri TARURA ikaongezewa mgao wa fedha, sasa hivi wanapata asilimia sijui 30, sijui 32 tukifika asilimia 40, TANROADS wakachukua asilimia 60 wale wakachukua 40 basi itasaidia sana katika kuweza kusimamia barabara mbalimbali zinazoenda katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu afya, nashukuru sana, naishukuru sana Serikali ilitupatia Mkoa wa Songwe kujenga Hospitali kubwa ya Rufaa ambayo inajengwa pale mpaka sasa hivi bado haijaanza. Naamini Serikali itachukua hatua kuhakikisha ile hospitali kubwa inaanza kufanya kazi. Lakini ile hospitali ni ya rufaa, tunahitaji tuwe na vituo vya afya, vituo vya afya katika Jimbo la Vwawa ambalo lina kata 18 tunavituo vya afya viwili tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba Mheshimiwa Waziri ikikupendeza basi Kata kama ya Ihanda ambayo inawakazi wengi sana tupatiwe kituo cha afya. Katika lile eneo ili kiweze kuhudumia wananchi wa Ihanda lakini pia na wasafiri wengi ambao wanaenda mpaka Tunduma wanapovuka mipaka kukiwa na ajali watakuwa na uwezo wa kupata huduma katika lile eneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Msia tunahitaji kituo cha afya lakini pale Hezya tunahitaji Kituo cha Afya, na Luanda tunahitaji Kituo cha Afya. Katika kipindi hiki tukiweza kupata Vituo vya Afya kama vinne au vitano vitatusaidia sana katika kuimarisha huduma za afya katika maeneo yale na mkipeleka na watumishi na madawa nina imani wananchi wa Jimbo la Vwawa wataendelea na uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nichangie kwenye upande wa elimu. Jimbo la Vwawa linashule za Sekondari zaidi ya 35. Tuna shule za msingi zaidi ya 90 katika Jimbo la Vwawa. Lakini shule za kidato cha tano ni chache, tuliomba katika kipindi kilichopita tukataka baadhi ya shule zipandishwe hadhi ili ziwe za kidato cha tano na ziweze kuchukua wanafunzi. Na katika hilo Serikali ilitoa fedha kidogo za kusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukapata Shule ya Msia, Shule ya Msia Sekondari ikapatiwa fedha kidogo kujenga madarasa. Shule ya Simbega Sekondari ikapatiwa fedha, lakini Mlangali ikapatiwa fedha yale majengo wananchi nao wakachangia matofali, wakachangia ujenzi wamejenga madarasa yamekamilika mpaka leo bado, bado zile shule hazijaanza kupokea wanafunzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba Watoto wetu wanahitaji kwenda kidato cha tano sasa ni vizuri basi hizi shule zikasajiriwa na zikapokea wanafunzi wa kidato cha tano mwaka huu watakaotoka maeneo mbalimbali tutakuwa tumechangia sana katika kuendeleza elimu ya Watoto wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia kuna watumishi wengi kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi ambao hawako katika mfumo wa malipo ya Serikali, wapo kwenye mikataba inakuwa ni mzigo mkubwa sana kwenye halmashauri na hii inatokana kwamba tulipoondoa wale madereva ambao hawana vyeti na watu wengine Halmashauri imebaki haina baadhi ya watumishi ikalazimika kwenye ajira za ndani. Hebu Mheshimiwa Waziri lifanyieni hili kazi ili nalo liweze kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambao ningependa nichangie ni kuhusu Mkoa wa Songwe, Mkoa wa Songwe ni Mkoa wa mwisho kuanzishwa hapa Tanzania ni mkoa mchanga pamoja na uwezo mkubwa sana wa kiuchumi. Lakini mkoa huu bado unahudumiwa na Mamlaka ya Mji Mdogo hatuna Halmashauri ya Mji, hatuna Manispaa limekuwa ni ombi la muda mrefu, tumeomba angalau tupate Manispaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Manispaa vigezo vitakuwa havijafikia basi tuangalieni kwenye Halmashauri ya Mji ili Mkoa kama Mkoa uwe na halmashauri ya kuweza kuwahudumia lakini kwa hali ilivyo sasa hivi hali si nzuri.

Mheshimiwa Waziri naomba hili mlipe uzito ili angalau Mkoa wa Songwe tupate Halmashauri ya Mji ama Manispaa ya Mkoa wa Songwe itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine tumeomba, tulimuomba Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli alipokuja tulimuomba eneo la kujenga soko, soko la mkakati, soko litakaoongeza mapato kwenye halmashauri. Akatukubalia lile eneo la kujenga soko likaanzishwa pale, ikatengwa eka hamsini pamoja na kujenga stendi ya Mkoa wa Songwe. Tunaomba haya yote yakapewe uzito unaostahili, mkayaweke katika mtazamo ili kusudi wananchi wale wa Jimbo la Vwawa wakaweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jambo la mwisho ambalo ningependa kuchangia katika siku ya leo ni kuhusu Wenyeviti wa Vitongoji na Mitaa. Hawa watu wanafanya kazi kubwa wanakutana na wananchi wanatatua kero nyingi wanashiriki kwenye maendeleo lakini hawana posho. Hebu wafikirieni hawa watendaji hawa itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo tuangalie Madiwani umefika wakati sasa Madiwani wawe na mshahara wa kudumu kuliko kutegemea kaposho. Wawe na wenyewe na mshahara hiyo itatusaidia sana kwasababu sisi Wabunge ili tuweze kufanya kazi tunawategemea sana Waheshimiwa Madiwani ili tuweze kushirikiana na kuchochea maendeleo kila mahali. Kwa hiyo nakuomba Mheshimiwa Waziri liangalieni hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mambo mengine mengi naamini Wizara ya TAMISEMI mtatekeleza majukumu yenu vizuri mtashirikiana, Wakurugenzi watatekekeleza majukumu yao nchi hii itaweza kusogea mbele na tutaweza kufikia maendeleo yale ambayo tunayatarajia.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba kusema kwamba, naomba kuunga mkono hoja. Nawashukuru sana kwa nafasi, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ili niweze kutoa mchango wangu. Nitajitahidi kutoa mchango kwenye maeneo karibu manne. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri Katibu Mkuu na timu nzima kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya katika kusimamia hii Wizara.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, naelewa kwamba Wizara hii ina majukumu mengi ambayo imepewa, lakini nadhani majukumu haya yamegawanywa kwenye makundi mawili; kuna suala la mipango, kuna masuala ya usimamizi wa fedha. Kwangu mimi napenda nishauri, Mheshimiwa Waziri wewe ni mtaalamu, hizi nafasi; mipango na fedha, usipoziangalia vizuri unaweza ukajikuta unatumia muda mwingi kwa asilimia 99 kwenye masuala ya usimamizi wa fedha, halafu ukasahau mipango. Ndiyo maana hata ukiangalia jina lako linavyoitwa, ni Waziri wa Fedha na Mipango. Wengine wanashauri ingekuwa Waziri wa Mipango na Fedha. Kwa sababu mipango ndiyo inayo-drive kuleta fedha. Sasa hilo ni la muhimu sana ukalitilia mkazo unapotekeleza majukumu yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naelewa tutakuwa na siku karibu saba za kujadili mipango na fedha na ukusanyaji wa mapato. Kwa hiyo, sitalisemea sana, bali nitazungumza maeneo mengine yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, wengi wamemzungumzia CAG na kazi zake na sina haja ya kurudia, lakini umuhimu wa CAG ni mkubwa mno. CAG ndiye anafanya kazi kwa niaba ya Bunge, ndiye anayeenda kuangalia bajeti tulizozipitisha kama kweli Serikali na taasisi zimetekeleza kama zilivyopitishwa na Bunge; ndiye anaenda kufanya ufuatiliaji kwa niaba ya Bunge, anakuja kutuletea ripoti; na kwa vigezo vya Kimataifa CAG anatakiwa awe huru, awe na rasilimali za kutosha, aweze kufanya kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunalo tatizo. Ukiangalia fedha anazopewa CAG kwa ajili ya kwenda kutekeleza majukumu ya kikatiba, yale ya kudhibiti na kukagua mahesabu ya Serikali; Idara zote, Wizara zote, Wakala zote, Balozi zote, nakadhalika, fedha ni kidogo sana. Hii nafikiri tuangalie mbele huko tunakokwenda namna tutakavyomwezesha CAG wetu aweze kupata rasilimali za kutosha ili akatekeleze majukumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi ukiangalia kwenye ripoti aliyoitoa, amesema amekagua mashirika 165, lakini mashirika hayako 165, yako zaidi ya hayo. Balozi hakukagua. Zote hazikukaguliwa na mambo mengine. Kwa hiyo, hatuwezi kuwa na uhakika juu ya matumizi ya fedha za Umma katika maeneo yote hayo. Kwa hiyo, ni vizuri tukamwezesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo lazima tumuandalie, tumpe uwezo wa rasilimali fedha na watumishi, hana watumishi wa kutosha huyu CAG ana watumishi wachache na watumishi wenyewe wengine hawana uzoefu wa kutosha, wengine hawajui hata zile kazi, ukiangalia kwenye bajeti hata ya CAG ya kuwajengea uwezo bajeti ni kidogo kwa hiyo, hata uwezo hawajengei, anawatuma kwenda kukagua wanaanza kuuliza huku wanamuuliza ndiyo waanze, ni kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nafikiri hili suala tuliangalie vizuri ili CAG, apewe rasilimali za kutosha lakini pia watumishi wa kutosha wenye uweledi akawajengee uwezo wafanye kazi ya kitaaluma ili heshima ya Bunge letu iwe kubwa, heshima ya nchi yetu iweze kupatikana hapo ndipo Utawala Bora utakuwa umeimarika nilidhani hiyo ni kitu muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kuwajengea huwezo unajua, anapowajengea CAG uwezo na Wabunge pia tutajengewa uwezo na ndiyo maana tunasema akijua kule na sisi atujengee uwezo ili atuambie anapo tuambia kule tuwe na uwezo sasa kujua kipi muhimu kipi siyo muhimu, kipi tuchukue hatua, kipi Bunge lifanye nini? Hiyo, itatusaidia sana katika kutekeleza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ambalo nilitaka kuchangia ni kwenye upande wa utoaji wa fedha za Serikali, fedha za maendeleo, fedha za maendeleo imekuwa ni kigezo na bahati nzuri umeshalisemea, hatuwezi tukawa tunapanga kila siku, tunapanga mipango mikubwa tunapitisha mabajeti makubwa ikija mwisho wa mwaka utekelezaji fedha zilizoenda sifuri, zilizoenda asilimia 10, zilizoenda asilimia 5. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa namna hiyo tutamuajibikashaje yule anayehusika na hiyo Taasisi au Wizara kwamba hakutekeleza hayo majukumu. Kwa hiyo, hili nadhani tutalijadili vizuri sana tutakapokuwa kwenye Bajeti Kuu na mipango tutakavyoliangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la nne ninalotaka kusema ni kuhusu usimamizi wa Fedha za Umma, usimamizi wa fedha za umma nitachangia kwenye maeneo mawili; la kwanza ni mifumo ambayo imetayarishwa, mifumo ambayo inayotakiwa kutayarishwa na Serikali kwa ajili ya kusimamia fedha za umma. Katika mifumo ambayo ipo sasa hivi dunia nzia inatumia teknolojia watu wamebuni mifumo mingi sana. Bahati mbaya kwa nchi yetu baadhi ya mifumo imekuwa ni mifumo inayotengenezwa kwa ajili ya kupiga Fedha za Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nadhani ni wajibu wa Wizara ya Fedha na Mipango kuhakikisha inakuja na mifumo itakayokuwa inaweza kusomana, itakayokuwa na uwezo wa kusimamia fedha za umma vizuri, haiwezekani mfumo huu hausomani na wa huku wala useme hivi mara useme hivi, hilo ni tatizo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili katika hilo la usimamizi wa fedha za umma tunaye mkaguzi wa ndani Internal Auditor General, Internal Auditor General kwa mujibu wa taratibu wa fedha, huyu ndiyo msimamizi wa kuhakikisha anakagua mifumo yote iliyoko kwenye taasisi kama inafanya kazi sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najua hata sisi Wabunge wengi hatuelewi tunafikiri CAG anaenda ku-discover fraud, anaenda kugundua wizi au ubadhilifu siyo kazi ya msingi wa CAG, siyo kazi yake. Kazi ya kugundua kama kuna ubadhilifu yaani kuna frauds kuna misappropriation, kuna errors in the books of account, mifumo haifanyi kazi ni kazi ya mfumo wa ndani ambayo ni ya Internal auditor. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa huyu internal auditor akiwa na uwezo wa kufanya kazi yake vizuri mifumo ikakaka vizuri CAG anapoenda pale kazi yake inakuwa ni nyepesi anaweza akatoa hata hati kwa kuangalita tu mifumo iliyoko pale akaridhika na kazi iliyofanyika. Kwa hiyo, ni vizuri huyu Internal auditor general akapewa uhuru…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, mumsikilize vizuri Mheshimiwa anavyotofautisha hivi vitu kwa sababu tuko baadhi yetu huwa tunachanganyaga hivi vitu, tunafikiri halmashauri ikipata hati sijui inamashaka au nini kwamba kuna wizi ndiyo anafafanua vizuri hakuna mwingine wizi wowote ni mifumo na mahesabu yalivyowekwa kihasibu nakadhalika, endelea Mheshimiwa kuweka vizuri. (Makofi)

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ahsante sana kwa ufafanuzi kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge ninachotaka kusema ni kwamba huyu mfumo wa ndani huyu Internal auditor general ndiyo muhimu kuliko hata CAG, ni muhimu mno kwa sababu yeye ndiye ataangalia kama kuna wizi, ataangalia kama kuna makosa, ataangalia mifumo kama inafanya kazi, ataangalia kama inasomana, ataangalia namna ya ku-share taarifa na kadhalika, hii ndiyo kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini bahati mbaya sana hatujamuwezesha vya kutosha hana watumishi wa kutosha na ukienda wale Internal auditor walioko kwenye halmashauri, walioko kwenye taasisi they are not independent hawaripoti kwake straight wanaripoti kwa wale watarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nataka niwaeleze danger iliyopo, huyu Internal auditor ameajiriwa yuko anaripoti kwa mkurugenzi akikuta mkurugenzi ametumia fedha vibaya na yeye kazi ya Internal auditor ni kumshauri mkurugenzi hata mshauri kwamba mzee hapa umekula au anafanyaje? Na huyo accounting officer anatuchua hatua? Hawezi hili ndiyo maana tukasema iazishwe office ya Internal auditor general na wale wakaguzi wote wa taasisi waende wakaripoti huko wafanye hiyo kazi kwa hiyo, nadhani ni kitu muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi mifumo yetu ni mibaya ukiangalia mahesabu yetu yanayofungwa kwenye halmashauri, kwenye taasisi hayakaa vizuri na kwanini hayajakaa vizuri? Kwa sababu watu hawajaelewa na bahati mbaya hatujaweka fungu la kuweza kuwajengea uwezo wahasibu wetu huko. Sasa hivi watu nafikiri ukimpeleka mhasibu kwenda kusoma ni kama unatupa fedha sasa matokeo yake…

SPIKA: Mheshimiwa nakupa dakika tano ufafanue hili jambo. (Makofi)

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana ninachotaka kusema wahasibu tunapoona taasisi fulani haijafunga mahesabu yake sawa sawa mahesabu yamekaa vizuri kwa kawaida siyo kazi ya mkurugenzi mkuu ni kazi ya wale wauhasibu, wasimamizi wa fedha wale. Sasa wale usipowajengea uwezo wasipojua International Account Standard wasipozijua, wasipojua International Auditing Standard watafanyaje kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana mahesabu yetu ukiangalia yamekaa kiajabuajabu kiukweli kuna wengine wamekuta huko yuko huko anasema ninauzoefu sana kwenye uhasibu, anasema unamiaka mingapi? Anasema anamiaka 25 kumbe alikuwa anaandika voucher tu miaka 25. Sasa miaka 25 alafu unauzoefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika sasa ukimpa kazi nenda kafunge mahesabu ni changamoto kubwa na Wizara ya Fedha, Mheshimiwa Waziri wahasibu wote wako chini yako, wahasabu wote nchi nzima wako chini ya Wizara ya Fedha, mwenye uwezo wa kuwajengea uwezo ni wewe, mwenye vyuo, vyuo vya Uhasibu viko chini yako. Sasa kinachoshindikana kuwajengea uwezo ili wafanye kazi nzuri, ili waitekeleze majukumu yao vizuri waitendee vema Taifa hili ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna IFM pale, una Tanzania Institute of Tanzania (TIA) unakile cha Arusha una vyuo vyote vya uhasibu viko chini yako. Mheshimiwa Waziri hebu wajengee uwezo hawa muwafundishe wajuwe hivi vitu wakafanye kazi na sisi tunakuwa tumefanya kazi vizuri naamini tunakuwa tumekwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona Mashirika mengi hayakushindwa kufunga mahesabu ni tatizo la mashirika yenyewe, wale viongozi wakuu ni tatizo la wale ambao wamekuwa charged na haya majukumu, unakuta kuna Director wa Financial, kuna Chief Accountant anaitwa CPA, mwambie afunge vitabu my friend, mwambie tu IPSAS wewe kamuulize tu IPSAS ina standard ngapi? Anakwambia ziko 42 ume-comply na zipi, anasema ngoja mpaka nikaingie kwenye mtandao, kama unajua utaingia kwenye mtandao vipi? Ukienda IFRS ina standard kibao, audit ina standard kibao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilitaka kusisitiza kwamba tukiwajengea uwezo hawa suala la utawala bora na usimamizi wa fedha za umma utaimarika vizuri sana na utakaa vizuri na hiyo itasaidia.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kama utaniruhusu ili nitalilema vizuri nitakapokwenda kwenye bajeti kwa sababu tunasema sasa hivi imefika mahali hizi Serikali za Mitaa zenye uwezo zinaweza zikafikiriwa kupewa zile tunaita dhamana treasury bonds zile municipal bond wakipewa zile kama wanakitu cha msingi cha kwenda kuzalisha na hawana fedha wanaweza kuruhusiwa kupewa, wakapewa dhamana ya miaka 10, miaka 15 wakakopa, wakafanya hicho na watakuwa na uwezo wa kujenga mambo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana na naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu upo katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni ukosefu wa mfumo wa kimenejimenti ambao ni unganishi (Integrated Land Management System). Mfumo huu utashirikisha Wizara karibu zote ambazo majukumu yao yanategemea kuwepo kwa ardhi ya kutosha. Kwa mfano Wizara ya Kilimo na Uvuvi, Nishati na Madini, Uchukuzi na Ujenzi, Viwanda na Biashara, Mazingira, Maji, Elimu na Afya. Mpango jumuishi ni muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu gharama kubwa za upimaji wa ardhi wakati teknolojia imeimarika, kuna haja ya kupunguza gharama ili watu wengi wapime ardhi, kwa hili itasaidia kuifanya ardhi kuwa mtaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kukua kwa miji bila ya mpangilio mzuri, hii inaleta bomoa bomoa katika maeneo mengi. Pia kuna haja ya kuongeza kasi ya kupima miji yetu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kwenye maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuimarisha utalii katika nchi yetu, nchi yetu ina vivutio vingi kama mbuga za wanyama, Mlima Kilimanjaro, maziwa na masalio ya kale. Serikali iongeze matangazo nchi za nje ili kuvutia watalii wengi zaidi pia usalama na amani ya nchi ni muhimu sana kuongeza hoteli na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna misitu mingi ambayo lazima ilindwe na kuvuna kwa utaratibu mzuri, haiwezekani nchi kukosa madawati katika shule zetu. Kuna wananchi wengi hasa katika maeneo ya Nanyara, Songwe na kadhalika wananyanyaswa sana na maliasili. Wengi wanapanda miti ambayo wanakata ili kuchomea chokaa, cha ajabu wanatozwa shilingi 15,000 kwa mti mmoja bila receipt naomba mfuatilie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimondo cha Ndolezi Mbozi ni muhimu kikajengewa fence ili kukihifadhi na kuimarisha utalii katika eneo hilo ni muhimu sana.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru wa kupata nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia machache ambayo ninayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nianze kwa kuzipongeza Kamati zote mbili kwa taarifa nzuri ambazo zimetolewa. Kwa kweli ni nzuri sana na naamini kama Serikali itazifanyia kazi basi hali itakuwa ni nzuri. (Makofi)
Mheshimwa Naibu Spika, suala la pili ambalo napenda kuchangia ni kuhusu taarifa za Mkaguzi Mkuu (CAG). Kwanza CAG ndiyo mwakilishi wa Bunge hili, ndiyo jicho la kwenda kuangalia kukoje huko katika taasisi zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitaenda haraka haraka kwa sababu ya muda, chukulia ripoti ya Serikali Kuu ya mwaka huu. Katika ripoti ya mwaka 2014/2015, katika Serikali Kuu taasisi 18 zilipata hati yenye mashaka na taasisi moja ilipata hati isiyoridhisha kwenye Serikali za Mitaa ndiyo inatisha. Ukiangalia kwenye Serikali za Mitaa mwaka 2011/2012 hati zenye mashaka zilikuwa 29, hati isiyoridhisha ilikuwa moja na hati chafu ilikuwa moja. Mwaka 2014/2015 kwenye Serikali za Mitaa ndiyo kunatisha, hati zenye mashaka 113, hati zisizoridhisha tatu na hati chafu moja, hii maana yake nini? Maana yake hali siyo nzuri katika taasisi zetu katika kusimamia fedha za umma na hapo lazima Serikali ichukue hatua stahiki kuhakikisha kwamba tunazuia hii hali ambayo ipo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hati yenye mashaka maana yake ni kwamba vitabu na hesabu zilizopo hazioneshi sura halisi ya taasisi. Sasa kama hivyo ndivyo ilivyo tusipochukua hatua hali itaendelea kuwa mbaya katika taasisi zetu. Naishauri Serikali yangu tuendelee kuchukua hatua stahiki ili tuhakikishe mambo yanakuwa mazuri katika miaka inayokuja.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tatu ambalo nataka nilizungumzie ni kuhusu taasisi chache ambazo zinafanya kazi kama TRA. Zipo taasisi ambazo zenyewe zinazalisha, zinafanya biashara, zinanunua raw material, zina-process goods halafu zinaenda kuzalisha zinauza kama TANESCO na zinginezo. Hata hivyo, zipo taasisi zinazofanya kazi kama TRA kwa mfano EWURA na TCRA hawana gharama zingine za uzalishaji zaidi ya tozo, zile tozo ni mali ya Serikali, lazima Serikali iweke mkono wake kuhakikisha kwamba zinaingia katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Hiyo ndio itakayoongeza mapato. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la nne, kwa sababu ya muda nakwenda haraka haraka lakini nizungumzie matatizo ambayo yamejitokeza. Labda niweke taarifa vizuri, nimesikia watu wameliongelea suala la Lugumi labda pengine niweke taarifa vizuri. Kwanza niseme mimi ndiyo nilikuwa Mwenyekiti wa Kamati Ndogo ya Lugumi iliyokuwa inashughulikia huo mkataba. Katika mkataba ule hadidu za rejea ilikuwa ni moja kwenda kuangalia kama ile mitambo ilinunuliwa na kufungwa, ndiyo ilikuwa kazi yetu. Hatukuwa na kazi nyingine zaidi ya hiyo na tulizunguka nchi nzima, Mikoa yote, Wilaya zote tukathibitishe kama zilinunuliwa na kufungwa. Naomba niweke rekodi sawa kwamba tulikuta kwa asilimia karibu 99 vilinunuliwa na kufungwa. Kilichokuwepo kwenye taarifa ya CAG alisema katika vituo vyote vile ni vituo 14 tu ndiyo mitambo ilikuwa inafanya kazi zake sawasawa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilithibitishie Bunge lako hili hata Kamati Ndogo ilipoenda ilikuta ni vituo 15 ndiyo vilikuwa vinafanya kazi yake sawasawa. Hiyo ndiyo iliyokuwepo kwenye ripoti ya Kamati yetu. Kama vituo 15 vinafanya kazi yake sawasawa kulikuwa na tatizo gani? Ile mitambo ina kazi tatu, kazi ya kwanza ilikuwa ni kuchukua picha na maelezo ya wahalifu; kazi ya pili ilikuwa ni kuhifadhi kumbukumbu zile kwenye njia ya electronic na kazi ya tatu ilikuwa ni kutuma sasa zile taarifa kwenye mitandao ili kuweza ku-share na vituo vingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka niliambie Bunge lako vizuri kwamba katika kazi ya kwanza na ya pili ilikuwa haihitaji kabisa mtandao wa internet. Hapa ndipo Kamati ilikuwa inauliza kama vifaa vyote hivi vilinunuliwa ni kwa nini sasa vilikuwa havitumiki kufanya kazi ya kwanza na ya pili, ndiyo swali lililokuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nilichotaka kusema ni kwamba mitambo yote ilinunuliwa, imewekwa lakini ilikuwa haijaanza kutumika. Hiyo ndiyo hoja ambayo tunayo kwenye Kamati na naomba ieleweke hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa muda huu.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi nami niweze kuchachangia bajeti hii. Jambo la kwanza nianze kabisa kwa kuunga mkono bajeti hii ambayo kwa kweli ni nzuri sana na yenye matarajio makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu yake kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya, kwa kweli Mungu awabariki, mnafanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wa Awamu ya Sita kwa namna alivyosikia kilio chetu, alivyosikia kelele zetu na kuamua kuja na bajeti ambayo inaenda kujibu yale yote ambayo tulimwomba. Katika bajeti hii tumefurahi kuona kwamba kwa mara ya kwanza tunakuja sasa na chanzo kingine kwa ajili ya ujenzi wa barabara za vijijini na mijini. Kwa kweli tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaenda kujibu hoja kubwa iliyokuwa inawasumbua Wabunge kwa muda mrefu kwamba tunaenda kutekeleza huduma ya bima kwa wananchi wote. Wabunge hawa walikuwa wanapata shida sana, wanapigiwa simu kila kona kwa ajili ya kutoa fedha kuwasaidia wananchi kwenda kupata matibabu. Sasa hii tukiitekeleza, itatusaidia sana kujibu zile hoja zetu. La tatu ni mikopo ya elimu ya juu na ya nne ni miradi ya vielelezo ambayo inaenda kutekelezwa. Hivi vyanzo kwa kweli ni vizuri sana. Kwa namna bajeti ilivyo, kwa namna alivyoileta, kwa kweli inatia moyo sana na inaleta matumaini makubwa sana, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu tulishatengeneza dira ambayo inaisha mwaka 2025 ambayo inataka maisha bora kwa kila Mtanzania ambayo tuliweka vigezo vyetu. Hapa takwimu zinaonyesha mambo mbalimbali ambayo Serikali imefanya. Nataka niseme kitu kimoja, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na Serikali ya Awamu ya Sita na Awamu Tano kwa kazi waliyoifanya. Kwa sababu kwa mara ya kwanza, naona kilimo kimeweza kukuwa zaidi ya wastani wa ukuaji wa uchumi wa Tanzania. Kwa sababu uchumi ulikua kwa asilimia 4.8, kilimo kilikuwa kwa asilimia 4.9. Hii ni mara ya kwanza, haijawahi kutokea. Kwa kweli hii tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaangalia pia mchango wa kilimo kwenye uchumi, umechangia asilimia 26.9. Sasa hizi fedha, nikizungumzia kilimo, tukazungumzia viwanda, ndiyo msingi mkubwa na ndiyo nguzo na ndiyo vitu ambavyo tumevipa kipaumbele katika kipindi hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema kwa mfano, viwanda vilikua kwa asilimia 4.5, mchango wake kwenye pato la Taifa ulikuwa asilimia 8.4, lakini ukiangalia mchango wa sekta nyingine; maji ilikuwa ni 0.5, umeme 0.3 na afya 1.4. Kwa hiyo, ina maana kuna sekta za muhimu ambazo zinachangia katika uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nitoe takwimu fupi. Ukiangalia ukuaji wa uchumi huu ambao tunao wa asilimia 4.8 bado wananchi wa kawaida hawawezi kuuelewa. Kwa nini? Kwa sababu mfumuko wa bei ni asilimia 3.3. Ongezeko la watu (population) ni asilimia 3.2. Ukizijumlisha kwa hesabu za kawaida unapata asilimia 6.5. Sasa kama hizo zote zinachukua asilimia 6.5 na uchumi unakuwa kwa asilimia 4.8 maana yake wananchi hawawezi kuona matokeo chanya ya ukuaji wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mantiki hiyo basi, lazima tuweke jitihada za kuongeza ukuaji wa uchumi, ukue zaidi ya asilimia 6.5 ndipo wananchi wa kawaida tutakapokuwa tunasema uchumi umekua na wataona kweli umekua kwa sababu hata mifukoni kwao utakuwa unaonekana. Bila hivyo itakuwa haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna umaskini bado ni asilimia 25.7. Riba kwenye mabenki ni asilimia 15.75, bado riba ziko juu. Ndiyo maana nampongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wa Awamu ya Sita kwa hotuba aliyoitoa kule Mwanza na hatua alizozisema kule Mwanza alipokuwa anafungua jengo la Benki Kuu, ndiyo msingi mkubwa wa hii bajeti. Ameagiza kwamba anataka riba kwenye mikopo ishuke na bila riba kushuka hatuwezi kujenga uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili linaendanda sanjari na hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Waziri wa Fedha amesema, hii hotuba lazima tufunge mikanda, nami nakubaliana kwa sababu ametekeleza sera zote mbili, anazitumia kwa wakati mmoja katika kuhakikisha anajenga uchumi. Anatumia Government expenditure na taxation, vyote amebana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kawaida ukibana, matokeo yake ni kwamba uchumi unaweza ukadorora. Sasa ili kusiwe na mdodoro wa uchumi lazima Benki Kuu ije na sera za fedha za kuhakikisha riba kwenye mabenki zinashuka ili kuhakikisha mzunguko wa fedha unaongezeka. Sasa hili naamini litakaa vizuri na Benki Kuu watakaa vizuri, kwa sababu kazi ya Benki Kuu ni kuangalia kila jambo ambalo Serikali inafanya na wao wanalisimamia kwa kutekeleza sera za fedha kwa kuangalia ile riba na mzunguko wa fedha. Hilo naamini wata-balance na ndiyo hapo uwekezaji na uchumi wetu utaweza kukua. Wasipofanya hivyo kutakuwa na mdororo wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo ya msingi ambayo nafikiri, kwa sababu hotuba hii imejibu karibu vitu vyote vingi, naomba nipendekeze mambo yafuatayo ili yamsaidie Mheshimiwa Waziri na kuhakikisha kwamba tunaenda sasa, tukimaliza hii miaka mitano, tunafika mahali pazuri zaidi. Jambo la kwanza napendekeza, Mheshimiwa Waziri ni vizuri ukarudisha ile Tume ya Mipango ambayo ilikuwepo. Kazi yake iwe sasa ni kufikiria vipaumbele, kuangalia vitu ambavyo nchi inaweza ikafanya, kuangalia namna ufuatiliaji na tathmini inavyotakiwa kufanyika ili utekelezaji wa bajeti na location ya resources ifanyike sawa sawa. Naamini hii tume itasaidia sana; na hii ndiyo takuwa na dialogue kubwa na kuwafanya watu wote waweze kushiriki katika mjadala mpana wa namna ya kujenga uchumi wa nchi yetu; (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ukiangalia sekta ya kilimo, ukiangalia viwanda, ukiangalia kwenye biashara, utaona tija bado iko chini sana. Mpaka sasa hivi hatuna chombo chochote katika nchi hii kinachozungumzia masuala ya tija, namna ya kuongeza tija, namna ya kuhakikisha kwamba tunapandisha uongezaji wa tija katika uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, nashauri mwangalie uwezekano wa wa kurudisha Baraza la Taifa la Tija ili lisaidie katika uchambuzi na kuhamasisha na kuwa na kampeni kali ya kuhamasisha na namna ya kuongeza tija katika kilimo, kwenye mifugo, uvuvi, viwanda, na kwenye huduma mbalimbali za uzalishaji. Hiyo itatusaidia sana, itatupeleka mahali ambapo ni pazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, tunazungumzia ujenzi wa SGR ambao utaenda kuchochea uzalishaji na kujenga uchumi wa nchi yetu hii. Nami napendekeza ile TAZARA upande wa nyanda za juu kusini, tunaitegemea sana. TAZARA ile mpaka sasa hivi ina uwezo wa kufanya kazi vizuri, lakini hatuna mabehewa ya kutosha na hatuna menejimenti ya kutosha. Kwa hiyo, ni vizuri Mheshimiwa Waziri mkaimarisha menejimenti ya lile shirika, mkaongeza mabehewa, yatachangia kwa kiwango kikubwa sana katika uchumi wa nyanda za juu kusini na hivyo tutakuwa tunaenda sambamba na huu ujenzi wa SGR ambayo tutajenga katika maeneo mengine. Nilidhani hiki ni kitu muhimu sana.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hasunga, kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba unavyozungumzia Shirika la Reli la TAZARA halina faida tu ndani ya nchi yetu, reli ile inaunganisha Tanzania na Zambia. Hivyo uchumi wa nchi hii ya Tanzania na Zambia tuna kitu kinaitwa kwenye uchumi comparative advantage. Yale ambayo hayapatikani Tanzania, tunayapata sisi Watanzania na yale yanayopatikana Tanzania hayapatikani Zambia wanayapata Wazambia. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hasunga.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo lakini nataka nimwambie kwamba TAZARA ni kitu muhimu sana kwa sababu kitasaidia kupunguza gharama za usafirishaji wa uzalishaji wa Mikoa za nyanda za juu. Kwa hiyo, kwa kuwa ina-connect na Zambia ndiyo maana tuliomba kwamba pale Tunduma, Mpemba tutengeneze bandari kavu ili mizigo yote SADC wawe wanakuja kuichukulia pale. Ikisafirishwa mpaka pale, naamini tutakuwa tumefanya vizuri sana katika uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne, nililokuwa nataka kupendekeza ni suala la kuongeza uwekezaji katika sekta za uzalishaji. Nimeangalia namna fedha zilivyotengwa kwa ajili ya kuongeza uzalishaji kwenye sekta za uzalishaji bado hatujaweka vizuri. Nafikiri Mheshimiwa Waziri mkalitafakari na kuliangalia kwa mapana na marefu. Hili litasaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tano, ambalo nataka niseme ni kuhusu sekta jumuifu ya masuala ya fedha. Sasa hivi kuna ukwasi kwenye mabenki. Mabenki mengi hayana uwezo wa kutoa mikopo kwa sababu hawana fedha za kutosha. Hii inatokana na kwamba mabenki mengi yame- concentrate mijini, yanatoa mikopo kwa watu wachache, watu walio wengi hawajajumuishwa katika mfumo jumuifu wa masuala ya fedha (financial inclusion).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo basi, katika jitihada ambazo Serikali ilikuwa imechukua na mkakati huu wa kuhakikisha kwamba sasa tunatumia teknolojia; mitandao hii ambayo inayo Vodacom, sijui Tigo na nini, imewafanya wananchi walio wengi sasa waweze kuingia katika sekta jumuifu ya masuala ya fedha. Sasa basi tunapokwenda ku- charge pale, inabidi tuchukue na tahadhari kidogo kwa sababu inaweza ikarudisha nyuma wananchi wengi kuwa katika mfumo jumuifu. Madhara yake ni nini? Kume-manage uchumi ambao ni informal, ambao hauko kwenye sekta rasmi, ni kazi kubwa sana. Tukijenga uchumi ambao ni formal, kila mtu yuko included, kila mtu anaweza ku-access mikopo, kila mtu anaweza kuwekeza, hiyo itatusaidia sana katika kuweza kujenga uchumi imara na kuweza kufikia malengo yale tunayokusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kusema kwamba Waziri Mkuu wa Singapore alipokutana na viongozi wa Afrika baada ya kustaafu mwaka 1992 aliulizwa, unafikiri ni vitu gani nchi za Afrika zinaweza kujifunza kutoka Singapore zikaendelea kama nyie mlivyoendelea kule Singapore? Sasa yeye alisema, ningekuwa Rais ya Afrika, ningekuja na mambo saba.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona bahati mbaya muda haukuwa kwangu, basi naunga mkono hoja. Nataka niseme, bajeti hii tuiunge mkono kwa kila namna, tumsaidie Rais, tuisaidie Serikali ya Awamu ya Sita, tukatekeleze miradi ya vielelezo ili tuweze kufikia malengo yanayokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Na mimi naomba nichukue nafasi hii kuchangia machache katika hii hotuba aliyoitoa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango katika hotuba zake mbili ya Hali ya Uchumi pamoja na Bajeti nzima ya Nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri na nianze kabisa kwa kuunga mkono hoja yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya mambo aliyoyazungumzia vizuri katika kitabu cha hali ya uchumi ni suala la kilimo, lakini kilimo kinaonekana kimekuwa kinakua kwa kiwango kidogo sana. Kilimo inaonekana kimekua kwa asilimia 2.3 ukilinganisha na sekta nyingine. Hii inatia wasiwasi wakati tumekuwa tukiimba kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo, kilimo ndiyo kila kitu, ndiyo kinatakiwa kuchangia kwa kiwango kikubwa Pato la Taifa, kilimo ndiyo kinaajiri zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania, kilimo ndicho ambacho kinaweza kikachangia katika kuimarisha thamani ya fedha yetu kwa kutuletea fedha za kigeni. Sasa hivi fedha zetu zimekuwa zikishuka thamani sana kwa muda mrefu ukilinganisha na dola, ni kwa sababu uzalishaji umekuwa siyo mzuri na mauzo yetu nje ya nchi yamekuwa siyo mazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo hiki kikiimarika kinaweze kusaidia vizuri sana ukiangalia katika hotuba zote tulizozitoa, ukiangalia katika maelezo yote aliyotoa tumeimba sana kilimo ni uti wa mgongo, lakini hakuna mikakati ya dhati inayoonekana kabisa kwamba kweli tunaenda kuiimarisha kilimo. Nataka kusema bila kuimarisha kilimo hii tunayosema uchumi umeimarika, umekuwa itakuwa ni hadithi, kwa sababu watu walio wengi asilimia kubwa wanategemea kilimo, bila kuwasaidia wao hizo sekta nyingine haziwagusi moja kwa moja. Kwa hiyo, ni lazima tuweke mikakati ya makusudi ya kuhakikisha kwamba kilimo kweli kinawekewa mikakati itakayosaidia kuimarisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kabisa ruzuku ambayo itatolewa kwenye pambejeo ni ndogo sana, sasa kama kweli tunataka kuimarisha kilimo tuongeze zuruku. Mimi nina uhakika kabisa Mikoa mingine ya Nyanda za Juu Kusini na hasa kwenye Jimbo langu la Vwawa wakulima wakipatiwa pembejeo za kutosha tutalima vizuri sana na tutazalisha kwa ziada nchi itapata ziada nyingi sana.
Kwa hiyo, ninaiomba Serikali iangalie upya sera ya kilimo ili kuhakikisha kwamba pembejeo zinafika kwa wakati na zinapatikana. Kilimo cha kahawa kiweze kufufuliwa, mahindi, pareto, tumbaku na mazao mengine yatachangia sana katika kuimarisha uchumi wa nchi hii. Hii kwa kweli haijanifurahisha kuona kwamba kilimo sasa hivi kimechangia kwa asilimia 2.3 tu wakati ndiYo kilikuwa kinaongoza kuliko sekta nyingine zote, hilo ni la msingi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo ningependa nichangie ni kuhusu Mfuko wa Maji Vijijini. Naipongeza Serikali imesema kwamba kutakuwepo na Mfuko wa Maji Vijijini na utaendelea kuwepo, lakini huu mfuko fedha ambazo zinapatikana zinaonekana bado ni ndogo. Sisi tungependa kabisa vijiji vyote vipate maji ili tuondokane na hili lazima tuje na mkakati wa makusudi kwa kipindi kifupi, iwezekane kabisa kipindi cha miaka miwili, mitatu tumalize kabisa hili tatizo la maji vijijini. Ili kumaliza hilo ni lazima tuweke tozo kwenye mafuta, kama tukiweka kwa mfano ikiwa shilingi mia tutapata fedha za kutosha kabisa zitakazoweza kusambaza maji katika vijiji vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tunaita Mfuko wa Maji, lakini hivi fedha nyingi zimekuwa zinatumika kwenye maendeleo ya maji mijini, kama ni za vijijini ziende kweli vijijini hiyo ndiyo itakayoweze kutusaidia na kuleta kweli kuinua hadhi. Mimi ninaamini kabisa kama maji tukiyasambaza vijijini wale wananachi wa vijijini maisha yao yatakuwa mazuri na watapata maji safi na salama na pia wataweze kulima hata kumwagilia bustani pale walipo katika maeneo yao itasaidia sana. Nafikiri hilo ni suala la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo ningependa nilizungumzie ni kuhusu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Kwa kweli niseme kabisa mimi nimesikitika na bajeti iliyotengwa kwa ajili ya ofisi hii, hii inatokana bajeti yetu imeongezeka! Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu ya Serikali anatakiwa kukagua Wizara zote, anatakiwa kukagua Idara zinazojitegemea zote, Wakala zote, Balozi zote, Mashirika ya Umma na haishii hapo tu anatakiwa kwenda kukagua miradi yote ambayo tumeipitisha. Ukiangalia kwenye bajeti yetu miradi ni mingi sana tunayoenda kuitekeleza, asilimia 40 ya bajeti inaenda kwenye miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tusipompa fedha za kutosha Mkaguzi nani atakayekwenda kufuatilia hiyo miradi na kuhakikisha kwamba hizo fedha kweli zimetekeleza yale ambayo tunayapitisha hapa Bungeni? Kwa hiyo, nashauri lazima iangaliwe upya ikiwezekana Mheshimiwa Waziri utakapokuwa unapitia upya mid year review ya bajeti lazima tuhakikishe Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali anapatiwa fedha za kutosha ili aweze kutekeleza majukumu yake ambayo yapo Kikatiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali hatakiwi uhuru wake kuingiliwa, kwa sasa hivi kinachojionesha ni kwamba atakuwa anaanza kuomba omba fedha na akianza kubembeleza kuomba fedha maana yake atakuwa na compromise independence yake, sasa hili ni suala ambalo lazima tuliangalie sana na huyu ndiye mwakilishi na ndiyo jicho la Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhakikisha kwamba inaisimamia ipasavyo Serikali. Kwa hiyo, naomba lazima hili suala liangaliwe vizuri ili angalau tuweze kwenda mbele, hili ni la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naelewa azma ya Waziri anayoisema, labda tuangalie Waziri je, mlipokagua mlikuta hela zake zinatumika vibaya? Kama mmekuta kwamba matumizi yake yalionekana mabaya basi ni sawa sawa. Lakini kama haijaonesha hivyo ni vema akapewa fedha za kutosha ili akafanye kazi ile ambayo tumeikusudia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa nichangie ni kuhusu kiinua mgongo cha Wabunge. Wenzangu wamechangia vizuri na mimi nisingependa nilisema sana. Nilitaka kusema sikuona sababu ya azma ya Serikali ya kulileta kwenye Bunge hili la kwanza kwa nini limeletwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, naelewa Kanuni za uhasibu za kimataifa zinavyosema, zinataka kiinua mgongo kitakacholipwa baada ya miaka mitano kinatakiwa kisambazwe katika miaka yote ambayo mfanyakazi ametumikia, yaani kama Mbunge ametumika kwa muda wa miaka mitano basi iwe prolated katika kipindi cha miaka mitano. Kwa hiyo, ina maana lazima ianze kuwa provided kwenye vitabu vya uhasibu kuanzia mwaka wa kwanza, hiyo azma naielewa, lakini haitakatwa kodi na haitatolewa, haiwezi kutolewa sasa hivi kwa sababu itakuja kutolewa mwaka wa mwisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuna sababu gani ya kuzungumzia masuala ya kodi kwa leo wakati hii kodi haitakatwa chochote mwaka huu? Kwa hiyo, hili suala kuna haja ya kuliangalia vizuri. Mimi nadhani hili linatuletea matatizo. Wenzangu wamelizungumzia vizuri nisingependa niliseme. Najua lazima liwe provided kwenye books of accounts, lakini lifanyiwe kazi vizuri ili li-cover wote wanaotakiwa kulipa kodi walipe, siyo tu iende kwa Wabunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine la mwisho ambalo ningependa nilichangie ni kuhusu shirika letu la ndege. Nimefurahishwa sana na Serikali kwamba tunataka sasa kulifufua shirika letu, lakini hili shirika lina madeni mengi sana na makubwa. Hizi fedha ambazo zimetengwa nisingependa ziende tena kwenye hili shirika, ningependa lianzishwe shirika lingine au hilo livunjwe lianzishwe lingine ndiyo lipewe hizo fedha na ndege tatu, hapo tutaweze kuona mchango halisi. Hizi fedha zikitolewa kama zilivyo mwisho zitaenda kulipa madeni mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na ninaunga mkono hoja. Ahsante.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-
(1) Mdororo wa uchumi umesababishwa na sera za uchumi wetu. Wakati Serikali imetumia sera zote mbili za fiscal policy kubana matumizi na kuongeza kodi katika bidhaa na huduma mbalimbali. Benki Kuu imekaa kimya kabisa bila kuchukua hatua zozote katika kupunguza riba za mabenki na kusimamia mzunguko wa fedha nchini. Hali hii ndiyo iliyosababisha mabenki kuporomoka na kushuka kwa uchumi. Fedha zimepungua kwenye mzunguko.
(2) Kupungua kwa uzalishaji bidhaa na kushuka kwa ajira nchini. Hivi sasa viwanda na makampuni mengi yameanza kupunguza wafanyakazi kama kwenye sekta ya utalii, hoteli na taasisi za elimu.
(3) Lazima Serikali ianze kurasimisha Sekta binafsi na kuziunga mkono ili zichangie katika pato la Taifa.
(4) Kuhamasisha kilimo kikubwa cha mazao ya chakula na biashara kwa kutoa support inayohitajika pamoja na masoko ya bidhaa.
(5) Kuendelea kuhakikisha kuwa Serikali inahamasisha na kusimamia sera ya elimu ikiwa ni pamoja na kuanzisha mitaala yetu ili iendane na mahitaji ya soko na kuongeza udahili ili nchi iwe ya wasomi wengi.
(6) Kuangalia vipaumbele ambavyo vina competitive advantages kufuatana na mazingira na jiografia ya nchi yetu. Lazima uchambuzi wa kina ufanyike. Kwa mfano; Bahari, Bandari, Mlima Kilimanjaro, Mbuga za Wanyama, Madini, Olduvai Gorge na kadhalika.
(7) Kuimarisha matumizi ya reli ya TAZARA ili kupunguza gharama za uzalishaji na uharibifu wa barabara katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ikiwa ni pamoja na kupambana na rushwa, ubabaishaji na kadhalika.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza Waziri Mkuu kwa kuja na hotuba nzuri. Naomba kuchangia maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ajira kwa vijana. Hivi sasa kuna vijana wengi ambao wamehitimu katika vyuo mbalimbali vya ngazi zote lakini kuna tatizo la vijana kukosa kazi za kuajiriwa ama kujiajiri wenyewe. Tatizo la ajira lina athari kubwa kiuchumi, kisiasa na kijamii. Lazima Serikali ije na mpango mahususi wa kuwaajiri au kuwawezesha kushiriki katika shughuli za kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo; hivi sasa kilimo kinaajiri watu zaidi ya asilimia 75; ili nchi iendelee lazima kutoa pembejeo kwa wakati na kwa bei nafuu. Ahadi ya Waziri Mkuu kuwa na bei elekezi ni muhimu sana. Lakini pia mbegu nzuri, kilimo cha kisasa na umwagiliaji ni lazima kwa
kipindi hiki. Baadhi ya maeneo tuanzishe mashamba makubwa ya kuanzia kilimo na kuleta tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, dawa za kulevya; naipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali za kupambana na dawa za kulevya. Ni muhimu vita hii iendelee kwa nguvu zote ili kuiokoa nchi, vijana na Taifa kwa ujumla. Naomba Serikali iongeze nguvu zaidi kuwakamata wauzaji, wasambazaji na watumiaji. Tungependa kusikia Kamishina wa Kupambana na Dawa aongeze kasi na kutupatia taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, rushwa; hivi sasa kuna rushwa sana katika maeneo ya Serikali za Mitaa kwa mfano Mbozi hali ni mbaya sana. Naomba vyombo vinavyohusika vichukue hatua za haraka kwani wananchi wanateseka sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nyingi zilizopo katika Jimbo la Vwawa zimekuwa hazipitiki kipindi cha masika. Tunaomba Serikali kupitia Mfuko wa Barabara kuzifanyia matengenezo ya mara kwa mara. Kuna barabara ya kilometa 10 alizoahidi Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni. Pia ili Mkoa mpya wa Songwe uunganishwe vizuri ni vyema Serikali ikajenga barabara zifuatazo kwa kiwango cha lami:-
(a) Barabara ya Njiapanda ya Iyula – Idiwili – Itezya hadi leje.
(b) Barabara ya Vwawa – Nyimbili – Hezya hadi Ileje.
(c) Barabara ya Viwawa - Igamba Magamba hadi Mkwajuni Songwe.
(d) Barabara ya Ihanda – Chindi hadi Chitete – Momba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuimarisha reli ya TAZARA ili iweze kutoa mchango mkubwa wa uchumi katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini. Hali ya Shirika hili si nzuri kabisa na wakati huo huo barabara nyingi zimekuwa zinaharibika sana kutokana na mizigo mikubwa. Ili kuimarisha kilimo, madini, ufugaji ni vizuri reli hii ikahudumiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa majengo ya ofisi na nyumba za watumishi katika Mkoa wa Songwe. Nini hasa mpango wa Serikali katika kujenga nyumba na majengo ya ofisi katika mkoa huo mpya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa huduma wa Wakala wa Umeme na Ufundi uimarishwe ili kutoa huduma nzuri za utengenezaji wa magari ya Serikali na umeme kwenye majengo ya Serikali. Hivi sasa gharama ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la TTCL na TCRA yaimarishwe ili yaweze kutoa mchango mkubwa katika utoaji huduma na kuchangia kukuza mapato ya nchi yetu. Ni vyema Serikali ikayasaidia zaidi.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu. Jambo la kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaendelea kuiongoza nchi hii na jinsi anavyoiweka kwenye ramani ya dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia hotuba aliyoitoa katika Umoja wa Mataifa, lakini tumeshuhudia pia hotuba aliyoitoa juzi; zote zimeleta matunda mazuri sana katika nchi yetu. Kwa kweli tunampongeza sana sana. Pia tunampongeza Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na pia Rais wa Zanzibar kwa namna wanavyoshirikiana katika kuziongoza nchi zetu hizi mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuleta Mwongozo huu wa Mpango na Bajeti wa mwaka 2022/2023. Kwa kweli ni mwongozo mzuri na ambao kwakweli nadhani tukiujazilizia jazilizia, basi unaweza ukaleta matunda mazuri sana. Hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Kamati ya Bajeti kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kuchambua Mpango huu, Mkakati huu na Frame Work hii na mpaka hapa walipofikia.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ya msingi ambayo kwa kweli yamezungumzwa katika Mpango huu na nimefurahi sana kuona dhima iliyoandikwa katika Mpango huu ambayo imeandikwa kwamba Kujenga Uchumi Shindani na wa Viwanda kwa Maendeleo ya Watu. Dhima imekaa vizuri sana, hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri, isipokuwa Dira bado sijaiona kwenye hii labda Mheshimiwa Waziri angeiweka na Dira, nayo ikakaa vizuri, short and clear itatuweka vizuri sana mahali pazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa yapo mambo ya msingi ambao Mpango wowote, Mwongozo wowote tunaoutoa na Mpango tutakaokwenda kuutekeleza, yapo mambo muhimu ambayo lazima Mpango wowote utakaokuja uende kuyajibu. Tutapenda Waziri atakapokuja na Mpango huo basi majibu halisi yapatikane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, jambo la kwanza ni umaskini uliokithiri katika maeneo mengi, Tanzania sasa hivi kuna umaskini mwingi. Sasa framework hii ituelekeze namna tutakavyoenda kukabiliana na umaskini wa nchi hii, umaskini wa watu walio wengi tutakavyoondokana nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni suala la ajira. Ajira kwa vijana wetu, ajira katika nchi hii ambayo imekuwa ni tatizo kubwa. Sasa lazima framework hii ituelekeze namna tutakavyoweza kutatua tatizo la ajira katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, ni ukuaji mdogo wa uchumi. Uchumi wetu hauendani na rasilimali tulizonazo, ukuaji wake bado upo chini sana. Sasa ni namna gani tunaenda kujipanga, tunakuja na mipango gani, tunatekeleza vipaumbele vipi na kwa namna gani ili uchumi ukue kwa kasi kubwa inayolingana na rasilimali tulizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hayo ni mambo muhimu ambayo tutapenda yawepo katika mpango ambao tunategemea uje. Kuna teknolojia duni ambayo imekuwepo katika nchi yetu, huduma duni katika maeneo mengi, lakini uongozi usiokuwa na maono katika baadhi ya maeneo. Sasa hivi Rais wetu na viongozi wa juu wana maono mazuri sana, mawaziri wana maono, lakini tuna tatizo la uongozi kutoka kwenye ngazi ya kati na kushuka chini. Sasa hili lazima tuliangalie vizuri, namna tutakavyoliweka vizuri ili sasa mambo yaende vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo pia tatizo la mapato kidogo ya Serikali. Ukiangalia mapato yetu ya Serikali sasa hivi makusanyo kwenye upande wa kodi ni asilimia 13 ya GDP na Mpango sasa hivi unaelekeza kwamba framework hii tutaenda kukusanya asilimia 16 ya Pato la Taifa. Sasa nadhani bado tupo chini ukilinganisha na nchi zingine zilizoendelea na nchi za wenzetu zinazoendelea kwa speed kali sana. Kwa hiyo ni muhimu tukayaangalia haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimeangalia uwiano wa ukuaji wa mchango wa Sekta mbalimbali katika uchumi wa Taifa letu. Nimeangalia kwa mfano ujenzi, ilikuwa kwa asilimia 9.1 na imetoa mchango kwenye pato la Taifa kwa asilimia 14.4; lakini ukichukua Uchukuzi imekuwa kwa asilimia 8.4 na imechangia kwa asilimia 7.5 kwenye pato la Taifa; Madini ilikuwa kwa asilimia 6.7 na imechangia kwa asilimia 6.7.

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya kwenye huu Muongozo haijaonyesha kilimo kilikuwa kwa asilimia ngapi? hili halijaonyeshwa, lakini imeonyeshwa mchango wa kilimo kwenye pato la Taifa ambao ni asilimia 26.9. Sasa kilimo kinatoa mchango mkubwa kwenye Pato la Taifa, lakini kilikuwa kwa kiwango gani na tuweke mikakati gani ili kilimo kikue kifikie katika kiwango tunachokitaka, hili nafikiri ni muhimu tukaliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia viwanda, biashara vyote hivi vimeonyeshwa mchango wake kwenye pato la Taifa, lakini vimekua kwa kiwango gani ili tutoke hapo sasa, Mpango utuelekeze tunataka tufike asilimia ngapi ya ukuaji ili tufikie malengo yetu, bado Mpango huu haukuweza kueleza. Sasa nafikiri hayo ni mambo muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia vile vile uwiano wa ugawaji wa rasilimali ambao tunaenda kuufanya sasa. Sekta zipo kama tatu; kuna Sekta za Uzalishaji ambazo ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi hii. La pili, kuna Sekta za Biashara na Huduma na sehemu ya tatu ni Huduma za Jamii. Sasa katika uzalishaji wote, lazima tuuangalie katika Mpango huo na katika Mpango unaokuja tuone rasilimali zinaenda kuwekeza kwa asilimia ngapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo swali ambalo tunajiuliza ni kiasi gani rasilimali zitatengwa kwenda kwenye Sekta za Uzalishaji na hasa kilimo ambacho kinaajiri watu wengi ambapo kwenye kilimo hapo ndiyo tunapata chakula chote, fedha za kigeni na wananchi wetu wanapata ajira yao, lakini ndiyo tunapata ajira nyingi kwa sababu ndio tunapata malighafi zote za viwandani, uchumi wetu kwa kiwango kikubwa unategemea kilimo. Sasa ukikichukua kilimo kwa mapana yake ndiyo unaweza ukatatua hata tatizo la umaskini na tatizo la ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namna gani tunaenda kufanya hilo ili kusudi tuone sasa sekta inatengewa kiasi gani, asilimia ngapi inatengwa kwa ajili ya kwenda kwenye sekta za uzalishaji, zikiungana na Sekta ya Uvuvi, Sekta ya Ufugaji, Sekta ya Madini, Viwanda, Utalii na Mazingira na hizo ndiyo sekta za uzalishaji, rasilimali kiasi gani zinaenda kutengwa kwa ajili ya kwenda kuongeza uzalishaji kwenye maeneo hayo. Tukiongeza uzalishaji kwenye maeneo hayo maana yake hata eneo la biashara litakaa vizuri, biashara itakaa vizuri, mambo mbalimbali ya biashara yatakwenda vizuri, lakini ndipo huduma za jamii tutakapokwenda kwenye maji, elimu, afya, ushauri na utafiti yatakaa vizuri. Sasa lazima tuwe na jedwali lile linaloonyesha mgawano wa hizo rasilimali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri tumefika mahali sasa tuweke malengo shabaha. Shabaha za kila sekta, tunataka sekta ya kilimo ikue kwa asilimia ngapi, ichangie kwa asilimia ngapi? Ili tunapofanya kazi tukajipime kwa kiwango hicho. Kama ni ufugaji tufanye hivyohivyo, kama ni biashara tufanye hivyohivyo, kama ni huduma tufanye hivyohivyo. Basi nafikiri hili litatusaidia sana katika kuweza kuimarisha ukuzaji wa uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naangalia mambo muhimu, nchi ya kwetu ndiyo pekee ina bahari, ina maziwa, bandari pale, hivi tutaimarishaje? Kwenye kilimo, upatikanaji wa mbegu. Sasa hivi hali ni mbaya, mbegu sasa hivi nimesikitika sana, mpaka leo tunapoongea mwezi Novemba Serikali bado haijatangaza hata bei za mbolea, haijatangaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezoea huwa wanatutangazia bei elekezi. Tunaponunua mbolea kwa mfuko wa pamoja huwa kunakuwa na bei elekezi, mpaka leo hazijatangazwa. Tunakwendaje kuzalisha, wakulima wa nchi hii wanakwendaje sasa kuzalisha, ambayo itaathiri kwa kiwango kikubwa maendeleo ya uchumi wa nchi yetu. Kwa hiyo, nilidhani kwamba hilo ni muhimu sana Mheshimiwa Waziri angeliangalia waone kitu ambacho kinaweza kufanyika ili kiweze kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona pia hali ya uchumi sasa hivi, kwa mfano mazingira yamebadilika, mvua hazijanyesha. Kule Mikoa ya Mbeya, Songwe, tunategemea sana mvua za mwezi Septemba na Oktoba kwa ajili ya zao la kahawa. Sasa hivi hazikunyesha, zimeanza kunyesha mwezi Novemba. Maana yake maua yote ya kahawa yameshaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mwaka mzima mwakani hatutaweza kupata kahawa ya kutosha. Sasa mkakati tunauwekaje ili kukabiliana na hii hali. Kwa hiyo, ninadhani ni maeneo muhimu sana ya kuyaangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie Reli ya TAZARA, itachangiaje kwenye uchumi. Siyo tu suala la kwamba hii reli inamilikiwa na nchi mbili, suala ni kwamba tunaongezaje mabehewa ya kuweza kusafirisha mizigo mbalimbali ili hii treni isaidie katika kukuza uchumi wa nchi yetu, hata kuishia pale mpakani tu. Tutajengaje pale kituo bandari kavu ili mizigo kutoka Dar es Salaam ifike pale nchi za SADC waje kuchukulia eneo hili. Nafikiri ni kitu ambacho lazima tukiangalie vizuri.

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. JAPHET N. HASUNGA - MAKAMU MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali, naomba kuchukua nafasi hii kutoa ufafanuzi wa hoja chache ambazo Waheshimiwa Wabunge wamechangia katika taarifa ambayo tuliwasilisha hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa na kwa moyo wa dhati, naomba kukushukuru wewe mwenyewe kwa kutoa muda wa kutosha kwa upande wa Bunge kuweza kuchambua taarifa ya CAG kwa undani. Pili, naomba kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita Mama yetu mpendwa, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa namna anavyoendelea kutafuta fedha na rasilimali mbalimbali ili ziweze kusaidia katika kuleta maendeleo ya nchi yetu, nampongeza sana. Tatu, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote ambao kwa namna mbalimbali wamechangia katika hoja hii ambayo tumeiwasilisha. Wabunge takribani 82 wamechangia, michango yao imesaidia sana kuboresha maazimio ambayo kwa kweli tutayaleta hapa Bungeni sasa.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii pia kuwashukuru Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa namna mbalimbali walivyochangia hizi hoja na fafanuzi mbalimbali ambazo wamezitoa. Kwa kweli tunawapongeza sana, wametoa ufafanuzi, wamenirahisishia ili niende moja kwa moja katika kusoma maazimio.

Mheshimiwa Spika, jukumu la kuisimamia Serikali ni jukumu la kikatiba, kwa mujibu wa Katiba yetu ukisoma ibara ya 63(2) ndio inayoelekeza Bunge hili kama chombo mahususi cha kuisimamia Serikali. Sambamba na hilo tunazo sheria, lakini tunazo kanuni zinazotuongoza katika kutekeleza majukumu yetu. Kamati yetu ya Hesabu za Serikali inazungumzwa pia katika Kanuni za Bunge ambapo katika Nyongeza ya Nane imeeleza mambo tunayotakiwa kuzingatia katika utekelezaji wa majukumu.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme hili ili Waheshimiwa Mawaziri watuelewe. Kwa mujibu wa Kanuni za Bunge mambo tunayoyaleta ndani ya Bunge ni maeneo ambayo yana matumizi mabaya ya fedha za umma. Kwa hiyo, yapo mambo mazuri ambayo yamefanywa kwa mujibu wa kanuni hatuyaleti hapa. Tunaelewa mambo mengi yanaendelea, lakini tunaleta yale yenye viasharia vya matumizi mabaya, hayo ndiyo tunayaleta humu Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachotuongoza katika kutekeleza majukumu yetu, tunaangalia Sheria za Fedha. Sheria ya Fedha ya mwaka ya mwaka 2001, marekebisho ya mwaka 2004 mpaka marekebisho ya mwaka 2020, inatuongoza kwa namna ambavyo fedha za umma na mali zinavyotakiwa kusimamiwa katika kila eneo na huo ndio msingi wa kuchambua hoja zetu humu ndani. Pia kanuni inatuelekeza, sisi Kamati ya PAC tunajadili mambo ambayo yamebainishwa katika ripoti ya CAG. Kwa hiyo, kama hayajabainishwa hatuwezi kuyajadili humu ndani, hivyo, tunayajadili haya, zipo Sheria za Manunuzi na sheria nyingine ambazo tunaendelea kuzizungumzia.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme kwa kifupi sana, wengi wamechangia utekelezaji wa maagizo ya Kamati, maazimio ya Bunge na hoja za CAG. Katika maeneo mengi bado utekelezaji wake ni hafifu na wajumbe wamechangia, nawapongeza sana wameliona kabisa na ndio uhalisia uliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna maeneo yenye udhaifu katika usimamizi wa fedha za umma. Sheria zipo, taratibu zipo, miongozo ipo, lakini watu wanakiuka kwa malengo yao na kwa nia zao. Nadhani hili halikubaliki.

Mheshimiwa Spika, kwa uamuzi uliouchukua kwamba sasa Bunge liisimamie Serikali, hapa maazimio, nataka niwahahkikishie Waheshimiwa Wabunge, nilisoma maazimio hapa, lakini sasa yanayokuja yatawezesha Bunge kuwa ni chombo kinachosimamia Serikali. Maazimio haya yamezingatia yale waliyoyasema ili Bunge kiwe chombo mahususi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye maeneo, yapo maeneo ya mifumo na Serikali kila siku hapa wanasema wanaenda kutengeneza mfumo mwingine. Nataka niliambie Bunge hili kuwa, eneo la mifumo ya TEHAMA linatumia fedha nyingi sana za umma na mifumo hiyo mingine wanatumia fedha nyingi halafu wanaiacha, wanakwenda tena kwenye mfumo mwingine. Ni eneo ambalo lazima litazamwe kwa mapana na marefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni eneo la manunuzi. Eneo la manunuzi ya vifaa na mali linatumia fedha nyingi na ni eneo ambalo ubadhirifu mwingi umekuwa ukitokea. Kwa hiyo hili eneo lazima liimarishwe. Kuna eneo la usimamizi wa mikataba, lakini yapo maeneo ya usimamizi wa ndani. Nataka niwaambie, bila kuwa na mfumo thabiti au mfumo madhubuti wa usimamizi wa ndani (internal controls), hizi hela zitaendelea kupigwa. Tuiombe Serikali waimarishe hiyo mifumo, itasaidia kupunguza ubadhirifu, rushwa na itasaidia kuhakikisha uzembe unapungua.

SPIKA: Mwenyekliti tuongoze vizuri hapo, umesema uiombe Serikali, ndio umeshaanza maazimio au ni jambo lingine? Maana sasa Wabunge tutakuwa hatuelewi hapa wakati tutakapokuwa tunahojiwa, kwenye hilo unalolisema azimio la Bunge ni nini? Yaani kama bado uko kwenye maelezo ya awali, sawa. Tuongoze vizuri, maana hatutaki kufika mahali tukawa hatujui Bunge linaamua nini?

MHE. JAPHET N. HASUNGA - MAKAMU MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, bado sijaanza maazimio. Kwa hiyo ni uchangiaji tu.

SPIKA: Kwa hiyo sasa unaleta maombi kwa Serikali?

MHE. JAPHET N HASUNGA, MAKAMU MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

Mheshimiwa Spika, labda katika maeneo machache nataka nitoe ufafanuzi kwa dakika chache. Kuna baadhi ya Waheshimiwa akiwemo Mheshimiwa Mpina alizungumzia suala la Deni la Taifa ambalo halikuonekana kwenye taarifa hiyo. Nataka niliambie Bunge lako kwamba, Kamati ilichambua Deni la Taifa, tuliangalia vigezo vyote na tuliangalie taarifa iliyopo, hakukubainika dosari zozote katika hilo, ndio maana kwenye ripoti hatujalileta. Vinavyokuja humu ni vile ambavyo vinaonekana ni madhaifu ya muda mrefu na ambayo yanaendelea kujirudia. Tulipoona hakuna hoja hatujaleta na ndio maana taasisi nyingi hatukuleta humu kwa sababu hatukubaini mapungufu kwenye hayo maeneo.

Mheshimiwa Spika, lipo eneo la KADCO, eneo hili nashukuru jinsi ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamelichambua na michango ya wajumbe imekuwa mizuri sana. Suala la Kamati lilikuwa kwamba kama wawekezaji, waliwekeza shilingi ngapi? Hapa ndiyo tulitaka Serikali watuambie, hawa wawekezaji waliokuja wakati huo wakaunda hiyo KADCO waliwekeza shilingi ngapi? Mpaka wakalipwa hiyo millioni 5.3, walilipwa kwa uwekezaji upi? Hilo ni suala la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili, tunataka kujua baada ya Serikali kuchukua mwaka 2010 mpaka leo KADCO imetekeleza mambo gani na fedha hizo za umma zimesimamiwaje? Bado hatujapata majibu ya hayo yote. Yapo mambo ya TPA na mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda naomba niende kwenye uchambuzi na mapendekezo ya maazimio moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo ya Kamati yametolewa kwa kuzingatia matokeo ya uchambuzi wa Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, mahojiano na Maafisa Masuuli pamoja na majadiliano na michango ya Waheshimiwa Wabunge iliyotolewa kuanzia tulipoanza kujadili tarehe 2-5 Novemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo hayo kwa kiasi kikubwa yatasaidia kuongeza uwajibikaji katika usimamizi wa fedha za umma kama ambavyo Bunge linatakiwa kusimamia na kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamesisitiza katika siku hizi nne za mjadala hapa Bungeni. Mapendekezo yanayoletwa mbele ya Bunge lako Tukufu ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja, azimio kuhusu nakisi ya Ukusanyaji wa Mapato kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA kiasi cha Shilingi trilioni 2.81: -

KWA KUWA taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali amebainisha kiasi cha Shilingi trilioni 2.81 cha mapato ambayo hayakukusanywa na Mamlaka ya Mapato (TRA) kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kutokana na mapungufu mbalimbali;

KWA HIYO BASI Bunge liazimie kwamba: -

(a) Serikali ifanye mapitio ya kina ya mfumo mzima wa ukusanyaji kodi (comprehensive tax regime review) ili kuhakikisha kodi zote zinakusanywa kama ambavyo Bunge linaidhinisha na kwa mujibu wa taratibu zetu.

(b) Serikali ifanye uchunguzi na kufanya hatua stahiki kwa watumishi wote wa Mamlaka ya Mapato Tanzania waliohusika kwa kukadiria kodi chini ya kiwango, kutoshughulikia madeni ya kodi kwa wakati, kuchelewa kusajili mapingamizi ya kodi kwa wakati, kutosimamia ushuru wa forodha kwenye bidhaa za mafuta na magari pamoja na usimamizi usioridhisha wa matumizi ya mashine za kielektroniki; hali iliyosababisha ongezeko la madeni ya kodi kwa zaidi ya 95% ndani ya mwaka huo wa fedha hivyo kuikosesha Serikali mapato ya kuhudumia wananchi.

Mheshimiwa Spika, mbili, azimio kuhusu dosari katika usimamizi wa mikataba na athari zake katika matumizi ya fedha za umma: -

KWA KUWA Kamati imebainisha upungufu katika uingiaji na usimamizi wa mikataba katika taasisi mbalimbali za Serikali hali iliyosababisha hasara kwa Serikali ikiwemo shilingi bilioni 68.7 kwa TANROAD, TANESCO dolla za Kimarekani milioni 153.43 na NFRA dola za Kimarekani milioni 33.4 na TPA bilioni 137.38;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali ifanye uchunguzi kubaini iwapo riba zilizotokana na mikataba ya ujenzi wa barabara katika TANROAD zilikuwa na uhalali na ulazima wa kuwepo? Hatua stahiki zichukuliwe kwa wahusika kwa kuzingatia matokeo ya uchunguzi huo. (Makofi)

(b) Serikali ichukue hatua stahiki kwa watumishi wa Wizara ya Nishati, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha na Mipango na TANESCO walioshiriki katika mchakato mzima wa uingiaji, usimamizi, utekelezaji na uvunjaji wa mikataba kati ya TANESCO na Symbion. (Makofi)

(c) Serikali ichukue hatua stahiki za kisheria kwa mkandarasi aliyechelewesha kukamilisha ujenzi wa ghati ya kuegesha meli katika Bandari ya Mtwara.

Mheshimiwa Spika, tatu, azimio kuhusu hali ya ukwasi kuhusu taasisi za kimkakati za Serikali (TPDC, TANESCO na STAMICO): -

KWA KUWA Taarifa ya CAG imebainisha changamoto za mtaji katika Mashirika ya Umma ya kimkakati kama TPDC, TANESCO na STAMICO;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina iongeze mtaji katika mashirika ya kimkakati ya Serikali kwa kufanya marekebisho ya msingi katika madeni ya taasisi hizo ili kuyageuza kuwa mtaji (equity). Pamoja na hatua hiyo, Serikali ihakikishe kuwa mikataba inayoingiwa na TANESCO, TPDC na STAMICO inakuwa na maslahi makubwa ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, nne, azimio kuhusu Ukaguzi maalum wa REA,Uhamiaji na Hombolo:

KWA KUWA Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, zimebainisha mambo muhimu katika kaguzi nne zilizopitiwa na kuchambuliwa na Kamati ambazo zimebainisha upungufu katika usimamizi wa fedha za umma;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali ichukue hatua za kisheria kwa Mkandarasi wa kampuni ya Derm Electric Tanzania Limited kwa udanganyifu na ubadhirifu pamoja na hatua za kisheria na kinidhamu kwa watumishi wa REA na TANESCO waliohusika kusimamia Mradi wa REA, awamu ya pili, Mkoa wa Mara, kwa kutotimiza majukumu yao ipasavyo.

(b) Serikali ichukue hatua za kisheria kwa watumishi 32 wa Idara ya Uhamiaji waliotajwa kuhusika katika mauzo ya sticker za Visa bandia katika Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Kilimanjaro kwa kuzingatia uhusika wa kila mmoja na matokeo ya ukaguzi maalum.

(c) Serikali ichukue hatua za kisheria kwa watumishi wawili waliojihusisha na ubadhirifu wa fedha za ada ya wanafunzi katika Chuo cha Serikali za Mitaa Hombolo.

Mheshimiwa Spika, kwenye ile (b), Mheshimiwa Waziri ametoa maelezo kwamba wameifanyia kazi, lakini sisi Kamati hadi tunachambua, juzi wakati wanakuja kwenye Kamati ni watumishi 11 tu ambao walikuwa wamepelekwa Mahakamani na hao 11 nao wote wamesharejeshwa. Kwa hiyo Waziri kusema kwamba hatua zilishachukuliwa, sisi kama Kamati mpaka juzi ilikuwa bado hatua hazijachukuliwa. Labda Waziri kama atatuambia kwamba hatua zimechukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tano, azimio kuhusu kutozingatiwa kwa Sheria ya Fedha za Umma, Sura ya 348:

KWA KUWA kupitia Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, Kamati imebaini ukiukwaji wa Sheria za Fedha za Umma, Sura 348 hivyo kuchangia upotevu wa fedha za Serikali;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia yafuatayo: -

(a) Shirika la Masoko Kariakoo, Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, afanye ukaguzi wa kiuchunguzi yaani (forensic audit) ili kubaini iwapo kuna ubadhirifu wa fedha za umma uliofanywa na kufichwa baada ya soko hilo kuungua moto. Aidha, vyombo vya dola vianze uchunguzi kwa uliokuwa uongozi wa Soko la Kariakoo ili kubaini iwapo wahusika wana jinai katika kuficha nyaraka za fedha kwa Wakaguzi.

(b) Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART). Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, aombwe kufanya ukaguzi maalum (special audit) wa malipo ya fidia ya kiasi cha bilioni moja na malipo ya fedha za usumbufu kiasi cha Shilingi milioni 434 yaliyofanyika DART ili kubaini iwapo yalifanyika kwa mujibu wa sheria.

(c) Mfuko wa Tozo na Tuzo wa Jeshi la Polisi, Fungu 28. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali afanye ukaguzi maalum (special audit) wa matumizi yote ya Mfuko wa Tozo na Tuzo wa Jeshi la Polisi tangu ulipoanzishwa na kisha kutoa taarifa yake kwa Bunge mapema iwezekanavyo. Aidha, Mlipaji Mkuu wa Serikali aandae kanuni za kusimamia uendeshaji wa Mfuko huo na malipo yote kutoka kwenye Mfuko yafanyike kwa kuzingatia kanuni zilizoandaliwa na Mlipaji Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, sita, azimio kuhusu umiliki na uendeshaji wa Kampuni ya Uendeshaji wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KADCO):

KWA KUWA mkataba wa uendeshaji wa uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro kati ya Serikali na Kampuni ya KADCO (concession agreement) unakosa misingi ya kisheria tangu mwaka 2010, wakati ambapo Serikali ilinunua hisa kwa asilimia 100 za KADCO baada ya malipo ya fedha za umma dola za Marekani milioni 5.3;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba Serikali irejeshe shughuli zote za uendeshaji wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege kama ambavyo inafanyika kwa viwanja vingine vya ndege hapa nchini kwa kuzingatia majukumu ya kisheria ya TAA na uamuzi wa Serikali uliokuwa umetolewa hapo awali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali afanye ukaguzi wa kina (comprehensive audit) wa mapato na matumizi ya KADCO kuanzia mwaka 2010 baada ya kuanza kumilikiwa kwa 100% na Serikali hadi sasa na Bunge lijulishwe ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, saba, azimio kuhusu utendaji wa kifedha wa benki za Serikali TCB na TIB:

KWA KUWA Taarifa ya CAG imebainisha kutokuwepo kwa mtaji wa kutosha wa benki ya Serikali za TIB na TCB, hivyo kukwamisha shughuli za benki husika na kuhatarisha fedha za umma zilizowekwa kwenye benki hizo;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba TCB na TIB zikusanywe mikopo yote ikiwa ni pamoja na kutaifisha mali za dhamana zilizowekwa na wakopaji husika kwa mujibu wa sheria ili kurejesha mtaji wa benki inayohusika.

Aidha, vyombo vya dola vifanye uchunguzi wa mikopo yote chechefu iliyotolewa na TIB na TCB ili kubaini iwapo ilitolewa kwa kuzingatia taratibu za kibenki na kuchukua hatua dhidi ya watu waliohusika.

(viii) Kuhusu ubadhirifu katika upanuzi wa Bandari ya Tanga.

KWA KUWA, Kamati ilifahamishwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwamba Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Tarehe 14 Juni, 2021 aliomba kufanyika kwa ukaguzi wa kiuchunguzi na kuainisha tuhuma za ubadhirifu wa fedha na matumizi mabaya ya madaraka uliofanywa na Watumishi wa TPA katika utoaji wa tuzo ya zabuni ya uboreshaji wa Bandari ya Tanga kwa Kampuni ya China Harbor Engineering Company Limited (Check). Ukaguzi huo umekamilika na kubaini ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma takribani Bilioni 65.3 ambayo ni hasara kwa Serikali; Na kwa kuzingatia masharti ya Kanuni ya 81(a) ya Kanuni za Ukaguzi wa Umma ya mwaka 2009, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU alipewa matokeo ya ukaguzi huo;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali ichukue hatua za kisheria kwa makampuni na Watumishi wote wa TPA waliotajwa katika taarifa ya ukaguzi maalum kwa kuhusika kwao katika ubadhirifu wa fedha za umma wakati wa utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa Bandari ya Tanga. (Makofi)

(ix) Kuharibika kwa dawa na kutokuwepo kwa dawa katika baadhi ya maeneo ya kutoa Huduma za Afya.

KWA KUWA, taarifa ya ukaguzi wa hesabu za Bohari ya Dawa (MSD), umebaini uwepo wa dawa zenye thamani ya Shilingi Bilioni 23.04 zilizokwisha muda wake zinatakiwa kuharibiwa. Pamoja na hilo ukaguzi umebaini kutokuwepo kwa dawa katika baadhi ya maeneo ya kutolea huduma za afya wakati ambapo kuna dawa zina maliza muda wake wa matumizi;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Bohari ya Dawa wasitoe dawa, vitendanishi au chanjo ambazo muda wake wa matumizi upo chini ya Miezi Sita ya kutumika yaani Shelf Life. Aidha, Serikali isipokee dawa, vitendanishi au chanjo za msaada ambazo pia muda wake wa matumizi upo chini ya Miezi Sita na kupelekwa MSD. Aidha MSD ipeleke dawa kwa wakati kwa wanao hitaji kwa maeneo yote ambayo wanakuwa wamepokea fedha zao. (Makofi)

(x) Mapitio na tathmini ya hesabu za Mifuko ya Hifadhi za Jamii.

KWA KUWA, uchambuzi wa taarifa ya CAG umebainisha kupungua kwa uwezo wa mifuko ya PSSSF kulipa mafao yake, pamoja na uwepo wa deni ambapo mifuko ya PSSSF na NSSF inadai kwa Serikali takribani Trilioni 1.5;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali iwasilishe Bungeni mpango wa malipo ya mikopo ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (Loan Repayment Schedule) kwa madeni yote ambayo mifuko inaidai Serikali. Mpango huo wa malipo uwasilishwe Bungeni kabla ya kukamilika kwa mwaka wa fedha 2022/2023. (Makofi)

(xi) Kuhusu mapungufu katika uzingatiaji wa Sheria za Manunuzi ya Umma na Kanuni zake.

KWA KUWA, taarifa za CAG zimebainisha kuwa baadhi ya Taasisi za Umma zimekiuka Sheria ya Manunuzi ya Umma na Kanuni zake hivyo kusababisha upotevu wa fedha za umma;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) ifanye ukaguzi wa kiuchunguzi katika manunuzi yenye dosari yaliyobainishwa na Kamati katika taasisi za TANESCO, Fungu Na. 57 Wizara ya Ulinzi, na kisha kuchukua hatua stahiki kwa kuzingatia matokeo ya uchunguzi. Aidha, TAKUKURU ianzishe uchunguzi wa wahusika waliofanya manunuzi bila kuzingatia sheria katika taasisi hizo na kuchukua hatua stahiki.

(xii) Kuhusu mapungufu katika mifumo ya udhibiti wa ndani.

KWA KUWA, taarifa ya CAG katika Mafungu mbalimbali zimebainisha mapungufu katika mifumo ya udhibiti wa ndani, hivyo kupelekea upotevu wa fedha za umma;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia;

(a) Serikali ichukue hatua za kisheria kwa watendaji na kampuni zilizohusika na ununuzi na usimikaji wa mifumo ambayo imeshindwa kufanya kazi kwa ufanisi katika Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA). Aidha, Kampuni hizo zifungiwe na Mamlaka ya Usimamizi wa Manunuzi Serikalini (PPRA) kujihusisha na shughuli za usimikaji wa mifumo hapa nchini.

(b) Bodi ya SUMA JKT, ichukue hatua za kinidhamu na kisheria kwa Watendaji waliokuwa wakisimamia mradi wa mauzo ya matrekta kwa kuruhusu uuzaji wa matrekta bila mikataba ya mauzo.

(xiii) Kuhusu taarifa ya ukaguzi wa ufanisi.

KWA KUWA, taarifa Nne za ukaguzi wa ufanisi zimebainisha masuala kadhaa katika taasisi za Serikali yanayohusu dosari katika usimamizi wa fedha za umma;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali afanye ukaguzi wa kina (Comprehensive Audit) katika mchakato mzima wa ugharamiaji, upangaji, utoaji na urejeshaji wa mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu. Aidha katika kipindi cha kila Miezi Mitatu Serikali ihakikishe inawasilisha Bungeni taarifa ya utekelezaji wa mapendekezo ya ukaguzi wa ufanisi yaliyotolewa na CAG kwa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, Tume ya Madini, TANROADS na BRELA.

(xiv) Usimamizi usioridhisha wa taarifa na huduma katika Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.

KWA KUWA, taarifa ya CAG imebainisha dosari katika usimamizi na udhibiti wa taarifa muhimu za wanufaika wa huduma za Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na gharama za matibabu ambapo pamoja na mambo mengine ilibaini utolewaji wa huduma za uzazi kwa upasuaji wa wanaume 731. Aidha ukaguzi ulibaini kuwa NHIF kukataa kulipa malipo ya Shilingi Bilioni 3.18 kwa hospitali za Serikali zilizotoa huduma kutokana na kuwa na mfumo wenye mapungufu, utambuzi na usimamizi wa taarifa;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali ifanye uchunguzi wa Idara ya Usimamizi na Udhibiti wa Huduma katika Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ili kubaini iwapo inatekeleza majukumu yake ipasavyo. Aidha uchunguzi ufanyike kubaini watoa huduma ambao wamekuwa wakiuhujumu Mfuko kwa kuongeza gharama za matibabu kwa njia ya udanganyifu na kisha kuchukua hatua stahiki kwa wote watakaobainika.

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kwa namna ya pekee kukushukuru wewe kwa namna ulivyosimamia mjadala wa taarifa za Kamati zinazotokana na taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao yenye tija na kujenga, ambayo imesaidia sana kuboresha mapendekezo ya maazimio ambayo yamewasilishwa hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna anavyoiongoza nchi yetu, lakini kwa namna anavyoifungua kiuchumi na kwa namna ambavyo ameamua kupanua demokrasia ya kweli, katika hatua hizi kwa kweli tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, nampongeza Makamu wa Rais pia, nampongeza pia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo anaifanya, lakini zaidi ya hapo nazipongeza Kamati zote tatu kwa taarifa ambazo wameziwasilisha humu ndani na uchambuzi wa kina ambao wameufanya kwa kweli nazipongeza sana Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kweli hotuba aliyoitoa humu Bungeni ime-set viwango vya juu sana, kwa sababu ime- cover maeneo yote, imechambua kwa undani maeneo yote ambayo yamefanyiwa kazi. Hii ni ishara tu ya mwaka mmoja ya Serikali ya Awamu ya Sita mambo ambayo imeyatekeleza, tukiendelea hivi kwa muda wa miaka minne ijayo nchi yetu itapiga hatua kubwa sana. Kwa hiyo mimi nawapongeza sana, naipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa ambayo wameifanya hapa tulipofika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona miradi mingi ya vielelezo, tumeona miradi mbalimbali, huduma za jamii kila mahali, kila eneo limeguswa katika mwaka huu tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo ambayo yamebaki ni mambo makubwa ambayo ni ya muhimu katika maendeleo ya nchi yetu, ambayo naamini kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inabidi itafute namna ambavyo tunaweza kufanya katika kutatua hizi changamoto. Changamoto ya kwanza ninayoiona ni tatizo la ajira kwa vijana wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tuna tatizo kubwa la ajira, vijana wengi wamesoma katika vyuo vikuu, wamesoma katika vyuo vya kati, wengi wana elimu lakini ajira imekuwa ni changamoto. Hali hii tusipoichukulia hatua, tusipoitafakari tukaja na mikakati ya kutosha litakuja kuwa ni bomu kubwa ambalo halitaisaidia nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nafikiri hiki ni kipindi pekee ambacho lazima tuangalie suala la ajira. Hili suala la ajira haliwezi kushughulikiwa na Serikali peke yake linahitaji sekta binafsi ambayo lazima iwe very strong ambayo ndiyo itaweza kuchukua vijana wengi wanaomaliza katika vyuo vyetu, tunahitaji kuwa na viwanda vingi na sekta mbalimbali zifanye vizuri ili ziweze kuajiri hawa vijana wengi ambao wamesoma katika taaluma mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali imeshasema tutatoa ajira zaidi ya 35,000, naipongeza sana Serikali kwa hatua hizo hongereni sana. Lakini hiyo itakuwa ni hatua moja, bado tunahitaji vijana wanaomaliza ni karibu takribani 90,000 mpaka 100,000 kwa mwaka, hiyo haitoshi. Pia sehemu wanayoenda kuajiri zaidi ni kwenye sekta ya Ualimu na Afya, zipo sehemu zingine, zipo taaluma zingine ambazo tunahitaji pia wawe na ajira, wanahitaji kutoa mchango mkubwa katika nchi yetu ambao bado ajira inaendelea kuwa tatizo. Kuna Wahasibu, kuna Wagavi, kuna Wahandisi, kuna Maafisa Utumishi na maeneo mengi kuna tatizo la ajira. Kwa hiyo, ninafikiri bado tunalo hilo tatizo ni lazima tulitafakari.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninashauri Serikali iangalie kwa namna ambavyo Mheshimiwa Waziri Mkuu ameratibu mambo mbalimbali, nashauri hata katika suala la ajira tuwe na mdahalo wa kitaifa wa kuzungumzia namna ya kutatua tatizo la ajira kwa vijana wetu ili kusudi Watanzania wote tushirikiane tuangalie kwa undani, tufanye nini ili kutoa ajira kwa Vijana wetu. Hiyo itatusaidia sana na tutaweza kujenga Taifa ambalo litakuwa linamanufaa na wataweza kufaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo ningependa kuchangia ni mishahara kwa Watumishi wa Umma. Katika kipindi cha takribani cha miaka mitano au Sita Watumishi wa Umma hawakuweza kuongezewa mishahara kwa sababu Serikali ilikuwa haina na uwezo, naamini tumefika mahali ili Watumishi wa Umma hawa waweze kufanya kazi yao vizuri, waweze kutekeleza majukumu mbalimbali, waweze kusimamia mipango mbalimbali ambayo Serikali inatakiwa kutekeleza wanahitaji pia kupewa motisha ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, Serikali sasa hivi iangalie namna itakavyoboresha maslahi ya Watumishi wa Umma. Ninalisema hivyo kwa sababu maslahi ya Watumishi wa Umma yakiboreshwa, wakiwa na mapato ya kutosha hawa pia watatoa ajira, kwa sababu hela wanazozipata wanaenda kuwekeza. Watawekeza kwenye kilimo, watawekeza kwenye miradi mbalimbali na ile miradi itatoa ajira kwa vijana mbalimbali. Kwa hiyo, zile pesa watakazozipata maslahi yakiboreshwa Watumishi wa Umma yataisaidia nchi katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali sasa ifike mahali katika Bajeti hii iwafikirie Watumishi wa Umma wote kuongezewa mishahara yao na nyongeza zile zinazotakiwa na maeneo mbalimbali ili maslahi na mazingira ya kazi yawe mazuri, yakiboreshwa mazingira ya kazi utendaji utakuwa mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni la msingi kwa sababu sasa hivi huko nyuma tulikuwa tunasema mteja ndiyo mfalme, sasa hivi wanasema rasilimali watu ndiyo mfalme katika Taasisi. Kwa hiyo, ukiimarisha hawa Watumishi wa Umma ukawapa motisha vizuri watakafanya kazi vizuri, watatekeleza malengo vizuri na nchi itapiga hatua kubwa. Kwa hiyo, napendekeza tuliangalie kwa makini suala hili la maslahi ya Watumishi wa Umma katika ngazi zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napendekeza tunapoangalia maslahi ya Watumishi wa Umma tuangalie na sekta binafsi, sekta binafsi sasa hivi tuna takribani miaka zaidi ya 13, kile kima cha chini cha mshahara havijawahi kurekebishwa kile cha kisheria. kisheria kima cha chini sekta zote hakijawahi kurekebishwa. Toka kimerekebishwa wakati huo kumetokea mabadiliko mengi, mfumuko wa bei, inflation rate imepanda sana, ukiangalia exchange rate, maisha yamebadilika. Fedha ambazo wanalipwa wafanyakazi wanaofanya sekta binafsi ni kidogo sana haziwawezeshi kuchangia katika Pato la Taifa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri ni vizuri Serikali sasa ikaangalia wafanyakazi wa sekta binafsi, na hasa kima cha chini cha sekta binafsi iwe ni kwenye kilimo, iwe ni kwenye uvuvi, iwe ni kwenye maeneo gani, maeneo yote ya sekta binafsi. Zipo sekta zaidi ya 12 ambazo tulipanga kima cha chini vya mishahara, sasa hivi kima cha chini sehemu nyingine tulisema ni shilingi laki moja toka mwaka 2013, tulisema Laki Moja mpaka leo wanalipa shilingi 100,000, hadi shilingi 150,000 ni nani anayeweza kuishi kwa kiwango hicho cha fedha? Ni wazi kabisa hawawezi katika kiwango hicho cha fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni vizuri Serikali sasa ikaliangalia hili ili hawa maslahi yao yakiimarika sekta binafsi ndipo uchumi wetu utaimarika, hawa watakuwa na uwezo wa kununua bidhaa zetu na wakinunua bidhaa zetu uchumi utakua.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kunaweza kukawa na bidhaa, kunaweza kukawa na huduma lakini watu hawawezi ku-access hivyo kwa sababu hawana uwezo wa kumudu namna ya kununua hivyo vitu. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikaliangalia hili suala la watumishi wa sekta binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo ningependa kulizingumzia ni kule Mkoani Songwe. Sasa hivi tunasema, bandari yetu hii, nchi nyingi zinatamani kuwa na Bandari kama ya Tanzania, lakini hazina hizo bandari. Sisi tunayo bandari na tuna maeneo mengi yenye bandari.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo, nchi ya Kongo imeingia kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki. Nchi zote za Afrika Mashariki zinajiandaa sasa kufanya biashara ya DRC. Sehemu pekee ambayo tunaweza tukafanya biashara yetu vizuri ni kuangalia uwezekano wa kufungua Bandari Kavu pale Tunduma. Tukifungua Bandari Kavu pale Tunduma, itasaidia wale wa Congo, Zambia, Zimbabwe na nchi nyingine waweze kusafirishea mizigo yao kupitia TAZARA mpaka pale Tunduma halafu wanakuja kuchukua mizigo pale. Watafanya vizuri sana na uchumi wetu utaimarika vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashauri Serikali, ni vizuri ikaangalia uwezekano wa kufungua Bandari Kavu lakini sambamba na hilo iimarishe TAZARA yetu. Sasa hivi TAZARA inafanya vibaya; na inafanya vibaya kwa sababu hatujaipa uzito unaostahili. Hili shirika toka limeanzishwa ni la nchi mbili; wenzetu upande mwingine inawezekana wasione manufaa ya kuimarisha hii TAZARA, lakini kwa nchi kama ya kwetu ambayo uzalishaji mkubwa upo kwenye Nyanda za Juu Kusini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri, ahsante.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, naipongeza Serikali kwa hatua zote hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata hii nafasi ili kuweza kuchangia katika taarifa hii ya Kamati. Kwanza naipongeza sana Kamati kwa taarifa nzuri ambayo wameiandaa ambayo na mimi pia ni Mjumbe wa hii Kamati, kwa hiyo nashukuru sana kwa taarifa nzuri hii.
Mheshimwa Mwenyekiti, tunapozungumzia maendeleo na tunapotaka maendeleo ya nchi lazima tuangalie ni vipaumbele gani ambavyo vitaashiria na vitafanya nchi ionekane imeendelea. Nasema hayo nikianzia na suala la kilimo. Katika kilimo asilimia zaidi ya 70 ya Watanzania wanategemea kilimo, nchi yetu hii tumesema tunataka sasa kujenga nchi ya viwanda, hatuwezi kujenga nchi ya viwanda, hatuwezi kukamilisha hilo kama hatutaimarisha kilimo. Viwanda vinategemea malighafi na malighafi hizo lazima zitoke kwenye kilimo. (Makofi)
Hata ukiangalia nchi za wenzetu, ukiangalia Ulaya industrial revolution ya Europe ilianzia kwanza na agricultural revolution, ilianzia kwanza na mapinduzi ya kilimo; mapinduzi yale ya kilimo yakaleta mapinduzi ya viwanda. Kwa hiyo, tunaposema maendeleo lazima tuweke tuzungumzie bayana kabisa, tuwe na mkakati wa makusudi wa kuimarisha kilimo chetu na ambacho ndicho kinatoa ajira kwa watu wengi, ambacho ndiyo kitatupatia malighafi za kutosha kwenda kwenye viwanda na kitachangia kwa kiwango kikubwa katika Pato la Taifa letu. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, hivi sasa kilimo chetu kinategemea mtu mmoja mmoja kilimo kidogo, hii haitatupeleka mbele kama Taifa. Lazima pia tuweke mkakati wa makusudi wa kuanzisha mashamba makubwa ya kilimo yatakayosaidia katika kuimarisha Pato la Taifa.
Mheshimwa Mwenyekiti, hivi sasa tunavyozungumzia kilimo nchi yetu sasa inakabiliwa na ukame katika maeneo mengi ambao tunaamini itaathiri kwa kiwango kikubwa sana maendeleo yetu ya kilimo. Mikoa ya Nyanda za Juu kama kule kwetu Songwe sasa hivi bado mvua zinanyesha na tena zinanyesha vizuri sana na wananchi wamelima mazao yanakwenda vizuri, tatizo lipo kwenye pembejeo, pembejeo sasa hivi kule Mkoani Songwe zimepanda vibaya sana. Katika kipindi cha nyuma Serikali ilitamka kwamba kwa mfano mbolea ya kukuzia ingeuzwa shilingi 26,000 lakini hivi leo ninapoongea pembejeo zimepanda sana kule Mbozi, mbolea ya kukuzia ni zaidi ya shilingi 50,000, sasa hii itasaidiaje? Hatuwezi kuendelea kwa namna hiyo. Kwa hiyo, naiomba Serikali itafute uwezekano wa kusaidia kilimo ili angalau tuweze kuinua pato la Taifa na kutoa ajira kwa wananchi walio wengi, hilo ni suala la kwanza.
Mheshimwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu usimamizi wa bajeti na nidhamu ya bajeti. Mimi nashukuru uchambuzi wa Kamati ulivyofanywa, lakini naomba nitoe ushauri wangu, fedha nyingi zinatoka kwenye Wizara ya Fedha, zinapopelekwa kwenye Serikali za Mitaa na kwenye taasisi za umma ni namna gani Serikali inasimamia na kufuatilia kwamba hizo fedha zinatumika kama zilivyopangwa, hilo ni suala la msingi sana.
Mheshimwa Mwenyekiti, pia kumekuwa na tabia kwamba katika baadhi ya maeneo watu wamekuwa wakibadilisha matumizi ya bajeti kinyume na Sheria ya Bajeti, hii siyo sawasawa. Mimi naamini Bunge baada ya kuidhinisha bajeti, bajeti inatakiwa itumike kama ilivyo na kama kuna mabadiliko basi hatua zinazoweza kuchukuliwa zifuatwe, kuliko sasa hivi mabadiliko ya bajeti yanatokea, bajeti tunapanga hapa inakuwa sasa haitekelezeki, kwa kweli hiyo itakuwa haitusaidii kama nchi, ni vema tukawa na msimamo na tukasimamia vizuri bajeti ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, lazima tuweke vipaumbele vichache vinavyoonekana kwamba kwa mwaka huu tunataka tuwe na kipaumbele gani? Tusichukue vipaumbele vingi, hiyo itatufanya kwamba tusionekane kama mwaka huu kipaumbele ni kusambaza maji tuhakikishe mwaka huu tunasimamia kusambaza maji. Kwa hiyo, bajeti ya maendeleo ilenge katika hayo maeneo, mwaka unaofuata tunaelekeza tena upande mwingine, hiyo, itatusaidia sana katika kuweza kuharakisha kuleta maendeleo na kuwa na nidhamu nzuri ya matumizi ya fedha.
Suala lingine ambalo ningependa kuchangia linahusu mapato yasiyotokana na kodi. Kwanza niipongeze Serikali kwa kuvuka malengo ya mapato yanayotokana na kodi kwa kweli naipongeza sana Serikali. Katika mapato ambayo hayatokani na kodi yaani non-tax revenues tumeweza kufikia asilimia 54; sasa asilimia 54 ni ndogo. Lazima tuwe na mikakati ya kutosha, tuchukue hatua zinazowezekana kuhakikisha kwamba tunaimarisha hili eneo maana lina vyanzo vingi, tunaweza tukapata mapato mengi.
Mheshimwa Mwenyekiti, ninaamini kama tukisimamia vizuri mashirika ya umma yakafanya kazi yao inavyotakiwa, yakafanya kazi kwa ufanisi, mashirika kama EWURA ambao wanakusanya fedha nyingi, mashirika kama TCRA, Civil Aviation, Reli, Shirika la Ndege na Bandari. Tukisimamia haya mashirika vizuri yataisaidia sana nchi hii kuweza kupata fedha na kupata mapato mengine yasiyokuwa yana kodi. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, nchi nyingi zinahitaji kuwa na bandari; sisi tuna bandari nzuri. Bandari yetu ile tukiimarisha nina uhakika kabisa tunaweza tukapata fedha nyingi sana na ikiwezekana mara mbili ya bajeti tuliyonayo, lazima tuweke mkakati wa kutosha katika kuhakikisha hilo eneo tunafikia malengo. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, nichangie pia kwenye eneo la ulipaji mzima wa kodi. Mimi naamini Watanzania lazima tuwe ni wazalendo wa kweli. Sasa hivi elimu ya mlipa kodi bado haitoshi, wananchi walio wengi bado elimu haitoshi ya ulipaji kodi. Katika maeneo mengi mimi nimeona pamoja na jitihada za Serikali, pamoja na mkazo ambao umekuwa ukitiliwa katika kukusanya kodi na watu kuwahamasisha maeneo mengi ukienda dukani mtu anakuuliza; nikupe risiti au nisikupe risiti? Risiti ni haki, risiti ni wajibu wa kila mtu kutoa na wanapopanga bei zao lazima wajue kwamba kuna wajibu wa kulipa kodi, kwa hiyo, lazima hilo lizingatiwe.
Mheshimwa Mwenyekiti, naiomba Wizara ya Fedha iweke mkakati kwamba, sisi Viongozi wa Siasa, Wizara ya Fedha na Serikali lazima tufanye jitihada za makusudi za kuhamasisha ili kuhakikisha kwamba wananchi wanapata elimu ya kulipa kodi, bila kulipa kodi hatuwezi kuleta maendeleo, tutakuwa tunaimba tu. Lazima wananchi wetu walipe kodi na lazima tuisimamie vizuri.
Mheshimwa Mwenyekiti, VAT (Value Added Tax) nina uhakika kama tutaisimamia vizuri itasaidia sana……
Mheshimwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipatia hii nafasi ili niweze kutoa mchango katika Wizara hii muhimu ambayo ndiyo imebeba maisha yetu. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na viongozi wengine wote wa Serikali. Lakini nawapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu nzima kwa kazi kubwa ambayo mnaifanya katika kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya elimu. Kwa kweli hongreni sana, sote tumeshuhudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yeyote ili iweze kuendelea inategemea uwezo wa watu wake katika kufikili, inategemea uwezo wa watu wake katika kuwa na maarifa ya kutosha, inategemea uwezo wa watu wake katika kuwa na ujuzi wa kutosha lakini katika kuwa na umahiri wa kuweza kutenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili hayo yaweze kutokea naomba ukisoma vitabu vitakatifu Hosea 4:6 unasema hivi “Watu wangu wana angamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako”. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inatukumbusha kwamba bila maarifa nchi hii hatuwezi kuendelea, bila maarifa ya kutosha umasikini wetu hauwezi kupungua, hauwezi kuisha, ili tuweze kupambana na umasikini, ili tuondekane na maradhi yaliyoko, ili tujenge uchumi imara, ili tuhakikishe kwamba tunakuwa na sayansi na teknolojia za kutosha hapa nchini tunahitaji maarifa, tunahitaji ujuzi wa kutosha na hii Wizara wamebeba hii dhamana ya kutupeleka huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri na timu yake yote na Makatibu Wakuu na wote tunawapongeza kwa mageuzi makubwa ambayo mmekuja nayo katika mwaka huu. Mmekuja na mageuzi makubwa kwanza bajeti imeongezeka na inazidi kuongezeka tumeona madarasa yanajengwa kila aina, vyuo vya ufundi vinajengwa hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko ya mitaala ndiyo kitu muhimu sana, ambacho mmekibeba na hiki mtaacha legacy katika nchi hii. Mabadiliko haya ya mitaala, mitaala yeyote lazima iendane na mahitaji ya nchi na agenda ya kitaifa ya nchi. Ajenda ya kitaifa ya nchi yetu sasa hivi ni umasikini uliokithiri, nikujenga uchumi imara ili tuweze kushindana katika nchi yetu hasa haya yote yatawezekana tukifanya mabadiliko makubwa ya mitaala yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wizara imeanza mabadiliko makubwa na ninawapongeza, juzi tumeshiriki hapa wametufundisha lakini wameleta watu 1,500 kuchangia mawazo kwenye mitaala, haijawahi kutokea mmefanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka Lee Kuan Yew wakati ananza kuitawala nchi ya Singapore aliitisha watalam, akasema nataka mniambie kama watalam nifanyaje ili nchi hii iendelee? Na wewe Mheshimiwa Waziri umesema jamani sisi mawazo yetu ni haya, nyinyi mna mawazo gani? Ndiyo maana umeitisha kila aina ya semina na watu kuchangia na sisi hapa tunachangia nakupongeza sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewasikia waliyochangia kuhusu kiswahili na waliyochangia kuhusu kingereza lakini mimi sitaki kuingia kwenye huo mjadala, nataka nikumbushe tu. Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Mwaka 1985 wakati anang’atuka, analihutubia Bunge hili nafikiri ulikuwa mwezi wa nane alisema hivi “kiswahili kimefanya kazi kubwa ya kuwaunganisha watanzania mpaka hapa tulipofika, akasema lakini kiswahili hakitatuwezesha kufika kule tunakotaka” sasa lazima tuzungumze kiswahili cha dunia, kiswahili kimetufikisha hapa sasa tuzungumze kiswahili cha dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda sitaweza kuyazungumza sana. Lakini kiswahili ni muhimu kimefanya kazi yake, kimetuunganisha watanzania sasa tutafute kiswahili cha dunia, ili tujifunze sayansi na teknolojia, iweze kutusaidi katika kujenga uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mageuzi yanayoendelea Mheshimiwa Waziri ya Mitaala, tunataka tuone kuwe sasa na mageuzi ya namna ya kufundisha. Ufundishaji wetu uendane na mitaala yenyewe tunayoihitaja. Vifaa tunavyovitaka kama ni competence based, umahiri lazima tuwe na vifaa vya kuhakikisha kwamba tunawaandaa vijana wetu katika hawa, hawawezi kufikia huko bila kuwa na vifaa vya kufundishia vya kisasa. Tunahitaji kubadilisha fikra, kwa sababu ukiwa na maarifa, ukawa na ujuzi bila kubadilisha tabia bado hatutaweza kufika, tubadilishe tabia maarifa hii itusaidie tuwe na nidhamu tuweze kutekeleza mambo yetu, tuweze kufanya kazi yetu vizuri, naamini hili linawezekana na kila kitu kitawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kazi mnayoifanya nzuri, vyuo vya ufundi, vyuo vya sekondari mnabadilisha manakarabati vya zamani mnakuja na mitaala mipya, mnakuja na vitabu vipya, mmesema mnaanza kufundisha walimu katika ngazi mbalimbali ili wawe ni competent hongera. Kwa hiyo, na sisi tutakuunga mkono kwa hali mali ili kuijenga nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Mkoa wa Songwe, Mkoa wa Songwe ni Mkoa wa Kilimo na unalima kweli kweli na tunachangia kwa kiwango kikubwa katika Taifa hili. Lakini tunazo shule za sekondari zaida ya 62 kwenye Wilaya ya Mbozi, Wilaya peke yake ya Mbozi yenye jimbo moja tunazo zaidi ya 62 shule za sekondari. Pamoja na kwamba sisi ni mkoa au ni wilaya ya kilimo lakini hatuna shule hata moja inayofundisha kilimo. Maana yake tunawaandaa wale watoto wasiende kwenye kilimo, kitu ambacho ni kizuri lakini je, kweli? Tuna uwezo wa kuwaondoa wote kwenye kilimo? Sasa hili Mheshimiwa Waziri naomba mliangalie, naomba hili mliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti namshukuru pia katika Mkoa wa Songwe ametuletea Chuo cha VETA. Unajenga chuo cha VETA sasa na nimeambiwa fedha zimeanza kwenda za kujenga Chuo cha VETA, tunapongeza sana kwa hilo, tunafurahia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema hata wakifanya vizuri bado maombi ayaishi, tunaendelea kuomba mkoa wetu ni mchanga ndiyo mkoa wa mwisho kuanzishwa hapa nchini, bado unamapungufu mengi, baada ya VETA tunahitaji tawi la chuo kikuu angalau kimoja, sasa hiyo iwe ni kutoka sekta binafsi, iwe ni kutoka wapi, tunahitaji chuo kikuu katika Mkoa wa Songwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo Mheshimiwa Waziri tumeona kazi ya kutoa elimu katika nchi hii ni kazi ya Serikali, lakini na wadau mbalimbali ambao wanachangia katika kutoa hiyo elimu ikiwemo sekta binafsi ambao kuna shule binafsi, kuna vyuo binafsi na kadhalika vyote vinachangia katika kutekeleza jukumu la kimsingi, la kikatiba, la Serikali yetu. Sasa basi vyuo hivi kusiwe na sera ya ubaguzi, hao watekelezaji wote waunganishwe, wanafanyakazi ileile ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi watoto waliyosoma kwenye vyuo, kwenye shule za sekondari za watu binafsi kwenye mikopo wanabaguliwa, wanaambiwa hawana uwezo hii siyo sahihi. Inatakiwa wale wasaidiwe, inatakiwa nao waungwe mkono ni watanzania, vyuo binafsi ni vyuo vya Tanzania. Kazi yetu sisi ni kuviimarisha, ni kuboresha mitaala vitoe maarifa mazuri, ili vivutie wasomaji na wanafunzi kutoka nchi za nje. Tupate watalii kutoka nchi za nje, waje kusoma Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa jitihada tulipofikia hapa, vyuo vyote vilivyoanzishwa hivi vinatakiwa vilindwe kwa sababu vinatoa ajira, vinatoa maarifa, vinachangia katika uchumi wa Taifa letu ili watu wengi kutoka nchi za SADC waje kusoma Tanzania, waje kuona Mlima Kilimanjaro, waje kuona bahari na maziwa waje kusoma hapa nchini kwa hiyo, ni muhimu tukaboresha katika hilo eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunahitaji vyuo vyetu sasa viwekeze kwenye kufanya utafiti na kutoa ushauri wa kitalamu. Sasa hivi kwenye vyuo vyetu mkazo uko kwenye kufundisha na kufundisha bado atujafikia kwenye level ya competence based, bado tunafundisha ya kinadharia zaidi. Sasa wakati tunatoka huko kwenda kwenye competence based lakini pia tusisitize kufanya utafi na tusisitize kutoa ushauri wa kitalamu na baada ya kufanya utafiti, tusisitize katika kuandaa machapisho ndiyo yatakayoisaidia nchi hii.

Mheshimiwa Mwwenyekiti, sasa hivi vijana wengi wanafanya project, vijana wengi wanafanya research nzuri sana unakuta anapata A lakini ukienda unakuta kwamba hiyo research aliyoifanya inaenda kuwekwa kwenye makabati badala ya kuichukua na kuona namna inavyoweza kuisaidia nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi, naunga mkono hoja, nasisitiza nawaunga kwakweli, tunawapongeza kwa kazi nzuri mnayofanya na nchi hii tunawategemea, maendeleo ya nchi hii yako mikononi mwenu Mungu awabariki, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa hii nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu, na nianze kwanza kwa kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa namna anavyofanya kazi na ambavyo amejitahidi sana katika kutafuta rasilimali fedha katika kutekeleza miradi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu kwa ujumla, kwa kazi kubwa ambayo kwa kweli mmeweza kutafsiri maono ya Mheshimiwa Rais na kuyatekeleza mambo mengi kwa kipindi kifupi. Kazi kubwa mmeifanya, mnastahiki kwa kweli kupongezwa, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaipongeza Wizara kwa sababu ya mambo yafuatayo ambayo yamejitokeza kwenye bajeti, sitaweza kuyasema yote, lakini machache naweza kuyasema.

Mheshimiwa Spika, kwanza, ongezeko la mapato yaani makusanyo yameongezeka kwa kipindi kilichopita mpaka sasa hivi. Mmefanya jitihada kubwa mapato yameongezeka, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuongezeka kwa bajeti za sekta za uzalishaji; kilimo, mifugo, uvuvi, bajeti imeongezeka kwa kiwango kikubwa. Haijawahi kutokea, kazi hiyo mmeifanya vizuri, hongereni sana na tunaona kwa mfano kilimo sasa hivi tena bajeti ya mwaka huu inaongezeka inakwenda kufikia shilingi bilioni 970. Kwa kweli hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mmeleta pendekezo la kuongeza shilingi 100 kwenye mafuta ili kuwa na vyanzo ambavyo vinaeleweka katika kutekeleza miradi ya kimkakati, hili ni jambo la msingi sana. Tunayo miradi mingi ya kimkakati, tulikuwa hatuna vyanzo, sasa hiki tukikifunga yaani tuka-ringfence itasaidia sana katika kutekeleza hii miradi ya kimkakati, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, TARURA imeongezewa fedha zaidi ya shilingi bilioni 370 zimeongezeka, lakini tumeshuhudia mapendekezo ya kwamba sasa vyuo vyetu vya ufundi, Chuo cha Dar Tech, Chuo cha MUST – Mbeya na Chuo cha Arusha, sasa watoto wote wanaosoma watapatiwa mikopo. Lengo tupate wataalamu katika nyanja mbalimbali, ni jitihada kubwa sana ambazo mmefanya, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mmesema mmetenga fedha kwa ajili ya kwenda kuchimba visima/mitambo ya kuchimba visima, hii kwa kweli itachochea sana maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, tumeanzisha Tume ya Mipango; tulishauri Tume ya Mipango ianzishwe, mmesikia kilio, kwa usikivu huo Tume ya Mipango imekwenda kuanza, hii ni hatua kubwa ambayo kwa kweli tumeifanya katika kipindi hiki na mambo mengine mengi ambayo mnakwenda kuyafanya. (Makofi)

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri na timu yako tunawapa hongera sana kwa kazi kubwa ambayo kwa kweli mmefanya. Yapo mengi ambayo yapo, hatuwezi kuyasema yote yakaisha, lakini mmeyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nichangie kwenye maeneo angalau mawili, kama muda utaruhusu nitaongezea labda la tatu.

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza ni suala la tija; tija kwenye kilimo, tija kwenye mifugo, tija kwenye uvuvi na maeneo mengine, lakini tija kwenye viwanda yetu. Tija bado iko chini sana, lazima tuweke mkakati wa kuongeza tija, tukiongeza tija ndipo pale tutaweza kupata ufanisi na ndipo uchumi wetu utaweza kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kilimo chetu ukiangalia tija ni ndogo mno, uzalishaji ni mdogo mno. Ukienda kwenye ufedhaji tija haipo kabisa. Sasa lazima kama Serikali tuwekeze rasilimali namna tutakavyosaidia kuongeza tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na katika eneo hili Mheshimiwa Waziri huko nyuma tulikuwa na Baraza la Taifa la Tija, sasa lile tuliliondoa. Sasa kwa kuwa Tume ya Mipango imerudi, basi napendekeza na hili Baraza la Taifa la Tija lirudishwe, lianzishwe ili lisaidie katika kuchochea na kuhamasisha kuongeza tija kwenye kilimo, mifugo, viwanda na huduma mablimbali na hii itatusaidia sana katika kujenga uchumi mzuri ambao utakuwa ni imara, naamini hili eneo mtalipa uzito unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu cha tatu ambacho nataka nichangie, sasa hivi sote tunazungumzia kilimo, mifugo na kadhalika, lakini hatuweki mkazo kwenye kuongeza thamani, value addition ya hizo. Hatuwezi kusema tuendelee kuzalisha malighafi, kuzalisha mazao tunauza nje, kufanya nini, sasa hivi dunia imetoka hapo, tujitahidi sasa uzalishaji wetu tuongeze thamani. Kwenye value chain hapa ndipo tunatakiwa tuwekeze sana. Tukifanya hivyo ndipo nchi yetu itaweza kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunazalisha mahindi tunapeleka kwenda kuuza mahindi yakiwa kama mahindi, tunazalisha kahawa tunakwenda kuuza kama kahawa, tuwekeze kwenye kuongeza thamani ya hivyo ili tukauze final products maeneo mbalimbali, na hiyo ndiyo itatusafanya kwamba tupate fedha nyingi, lakini pia uchumi wetu uwe imara na ajira mbalimbali ziongezeke na umaskini katika nchi yetu uweze kupungua. Kwa hiyo, mimi napendekeza hebu tuangalie sana value addition katika products zetu, tukiwekeza hapo itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nilitaka kuchangia na nilitaka kuongeza, kwamba nimeona katika jitihada mbalimbali ambazo zimechukuliwa na Serikali na nimeona kabisa kwamba kwa kweli jitihada ni nyingi zinachukuliwa. Lakini mimi nataka tulipendekeza hapa kipindi kilichopita kwamba katika ufufuaji na uimarishaji wa bandari zetu, tukasema tunataka na Bandari ya Bagamoyo sasa tuijenge, tulipendekeza mwaka jana tukasema ijengwe.

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye hili sijaona mkakati wa kusema sasa tunaanza mikakati ya kuijenga Bandari ya Bagamoyo, kwa sababu hii ni rasilimali tuliyopewa na Mwenyezi Mungu. Tunataka zile bandari ziweze kuhudumia maeneo mengine. Tukiimarisha miundombinu hii ya SGR, barabara na maeneo mengine, tunataka sasa bidhaa zisafiri vizuri tuwahudumie nchi za SADC zote, nchi za Kusini mwa Afrika ambazo sisi tuna lango hili kwenye bahari yetu tuweze kuitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi nataka nione mkakati, tuna mkakati gani wa kuhakikisha tunatafuta kama ni mwekezaji, kama ni nini, tujenge Bandari ya Bagamoyo ili ishirikiane na bandari zilizopo katika kuweza kuchangia uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sanjari na hilo, pale Tunduma bado naendelea kilio changu, pale ndiyo lango la SADC, tunaomba pawe na bandari kavu, bandari kavu ile itasaidia sana katika kuweza kutoa huduma katika nchi za SADC, mizigo itasafirishwa kutoka kwenye Bandari ya Dar es Salaam na bandari nyingine, ikifika pale basi wale wafanyabiashara watachukua kwa gharama nafuu kuliko namna sasa hivi inavyosafirishwa kwa kutumia magari na barabara zinaharibika na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, lakini zaidi hapo tunaomba mkakati mahususi wa kuimarisha reli ya TAZARA. Reli ya TAZARA ilijengwa ni reli ya uhuru, reli ya siku nyingi, reli ambayo ni muhimu sana katika uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, mlituahidi kuleta sheria hapa kwamba mtabadilisha sasa sheria ili ile TAZARA ambayo inamilikiwa na nchi mbili iweze kuboreshwa, tuweze kuwekeza, iweze kutoa mchango mkubwa. Sasa mpaka sasa hivi sijasikia nini kinaendelea kuhusiana na ufufuaji wa reli ya TAZARA. Tunataka tupate mwelekeo wa Serikali ni nini katika kuhakikisha kwamba kwa kweli tunaifufua TAZARA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, TAZAMA Pipeline ya kusafirisha mafuta nayo ni ya nchi mbili. Tumekuwa tukisafirisha yanakwenda Zambia, sasa hivi wameanza kusafirisha mafuta safi. Sasa mkakati wa Serikali uwepo ili ile TAZAMA Pipeline tusafirishe mafuta kutoka Dar es Salaam, yakifika Mbeya iwepo depot pale, yakifika Tunduma iwepo pale tupunguze gharama za uzalishaji, gharama za ongezeko la mafuta, gharama zile zitapungua, tukiweka pale yatasukumwa kwa TAZAMA, yatafika pale, yatapakuliwa na wafanyabiashara mbalimbali watachukua mafuta katika yale maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi naamini kwamba tukifanya hivyo itatusaidia sana katika kuweza kujenga uchumi wetu imara katika maeneo hayo, lakini pia tutapunguza gharama kwa watumiaji wa mafuta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zaidi ya hapo, napendekeza kuanzisha Mfuko wa Kuchochea Ujenzi wa Viwanda. Hatuwezi kuendelea kuimba tu tukasema uchumi wa viwanda, lazima tuwe na mechanism namna tutakavyochochea. Maeneo mengine tunajenga viwanda tukivikamilisha ndiyo tunatafuta mwekezaji wa kuviendesha vile viwanda, na ndipo hapo tutakapoweza kuvutia watu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Waziri, naiomba Serikali, kuhakikisha kwa kweli tunakwenda kwenye uchumi mpana, uchumi mkubwa, jitihada nzuri mmezifanya, tumeona. Sasa Mheshimiwa Waziri hapa utatusaidia kutupa majibu maana yake ukisoma kwenye taarifa yako, mwaka 2021 unasema pato la Taifa kwa nchi yetu kwa dola za Marekani ulikuwa bilioni 69.9, mwaka 2021; mwaka 2023 tunategemea itakuwa bilioni 85.5. Uki-calculate pale, ukipiga hesabu ukuaji ni zaidi karibu toka mwaka 2021 Serikali ilipoingia Awamu ya Sita hii toka wakati huo ni zaidi ya asilimia 22, ukitoa unakuta kwamba yaani kwa kweli growth rate ingekuwa ni kubwa zaidi ya pale.

Mheshimiwa Spika, sasa hebu utatusaidia, ni nini hasa ambacho kipo katika calculations. Kwa sababu IMF ndiyo wametoa hizo takwimu kwamba uchumi pato limetoka hapa limekwenda hapa, sasa ku-calculate kwa kawaida haitupi hii figure ambayo mnaisema, inaonekana nchi tumefanya vizuri zaidi kwenye uchumi kuliko ambavyo takwimu zinaonekana kwenye madaftari. Kwa hiyo, mimi nafikiri kwamba ni suala la kujipongeza, ni suala la kusema tumefanya hapa tuongeze nguvu zaidi ili mambo yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja na ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali wa Mwaka 2016
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kuja na miswada hii miwili ambayo ni miswada muhimu sana na ambayo tumekuwa tukiisubiri kwa muda mrefu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia naipongeza Kamati ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa jinsi ambavyo imeuchambua huu muswada pamoja na Kambi ya Upinzani.
Mheshimiwa Naibu Spika, muswada huu utaleta manufaa mengi sana katika nchi yetu. Kwanza tunaamini kabisa kwamba matokeo ya uchunguzi wa kikemia sasa utakuwa na msemaji mkuu na utakuwa na hadhi inayostahili ndani ya nchi na pia nje ya nchi kwa sababu sasa utalindwa na sheria hii ambayo tunaenda kuitunga.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, kuanzishwa kwa kamati za kitaaluma ambazo zinashirikisha wadau wa aina mbalimbali, hili ni suala ambali ni la msingi sana na huu muswada utatusaidia sana katika kutatua matatizo mbalimbali ambayo yamekuwepo. Lakini pia katika muswada huu tunaona wakaguzi wa maabara watateuliwa na kupewa kazi za kufanya. Wamewekewa mipaka, wamewekewa maslahi yao, lakini pia wamewekewa mipaka na maeneo ambapo wataishia katika kutekeleza majukumu yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika muswada huu tunaona sasa unatamka bayana kwamba maabara zote nchini itakuwa lazima zisajiliwe na sasa zitakuwa zinasajiliwa na kutambulika kisheria. Hiyo itatuwezesha kuondokana na matatizo mbalimbali ambayo yamekuwepo, na uholela ambao umekuwepo katika utengenezaji wa kemikali katika maeneo mengi, na hivyo wananchi wataweza kunufaika na muswada huu na miongozo ambayo itakuwa imetolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kwanza nichangie katika baadhi ya vifungu hivi vya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali. Nianze na hivyo na kama muda utaruhusu nitaenda sehemu nyingine. Kwanza nianze na hili la kwanza la idadi ya wajumbe.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama mchango wangu wa jumla, kwanza mimi nakubaliana kabisa kwamba bado Mheshimiwa Waziri apewe mamlaka ya kufanya uteuzi wa Wajumbe wa Bodi, hilo sina matatizo nalo kabisa. Lakini mimi kitu ambacho natofautiana, idadi ya Wajumbe wa Bodi ni kubwa mno katika hizi taasisi za umma. Katika huu muswada inaonekana wanatamka kwamba Wajumbe wa Bodi watakuwa sita, ukijumlisha na Mwenyekiti, pamoja na Mkemia Mkuu, watakuwa wanane. Mimi idadi hiyo naiona ni kubwa sana. Hii inaongeza mzigo wa uendeshaji wa mamlaka. Bodi nyingi ukiangalia ziko sita, saba, nane, mimi nashauri muswada huu ungekuwa na Wajumbe wa Bodi wanne, ukawa na Mwenyekiti na Msajili wanakuwa sita maximum; wanatosaha kabisa kuweza kutekeleza majukumu ambayo yameainishwa kwa mujibu wa sheria hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tunaona katika katika hii Bodi ya Mamlaka ambayo itafanya majukumu mengi yenye wadau wengi inachukua zaidi wajumbe kutoka kwenye Serikali na taasisi zake. Mimi nadhani kuna haja ya kuhakikisha kwamba sekta binafsi nao wanakuwemo katika hii mamlaka. Na hii sekta binafsi tunaweza tukaangala kwa mfano, wawakilishi kutoka labda waajiri yaani ATE kule wanaweza wakaleta mtu mmoja akawakilisha wale wadau wa sekta binafsi au kutoka Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi; kukawa na mwakilishi huko anaeweza kutusaidia pia katika kuleta mchango na kuchangia katika hii mamlaka na hivyo kutetea maslahi ya hii sekta binafsi; hilo ni suala nafikiri ambalo lingeweza kusaidia sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine katika hizi Bodi naona katika hii Sheria wameweka kwamba akidi katika mkutano ni theluthi mbili. Theluthi mbili ni kubwa sana. Hiyo itafanya baadhi ya vikao vingi viwe vinaahirishwa; na wale Wajumbe ambao wanakuwa wamefika siku hiyo ukiahirisha kikao unakuwa umeshawahribia ratiba. Kwa hiyo, katika Bodi mimi nashauri wangeweka akidi iwe ni nusu badala ya theluthi mbili. Nusu ya Wajumbe inatosha kabisa kuweza kuhakikisha kwamba wanashiriki na wanafanya kikao halali kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika kifungu cha 8(1) kinataja majukumu ya bodi. Majukumu hayo ambayo yanatajwa ukiangalia ni majukumu mazuri tu yameainishwa vizuri sana. Lakini kuna baadhi ya majukumu ambayo yametajwa pale mimi nilikuwa nadhani katika kifungu (h) na (j) nadhani hii kazi pengine iliandikwa labda kwa uharaka zaidi hawakuliangalia vizuri. Najua Mkemi Mkuu wa Serikali ilikuwa ni wakala wa Serikali, na ukishakuwa wakala unakuwa na bodi ambayo tunaiita ni Ministerial Advisory Board, kwa ajili ya kumshauri Waziri ili aweze kufanya maamuzi ya kimkakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, naona bado katika hizi kazi za bodi wameandika hivyo hivyo. Pale kwenye (h) wameandika itamshauri Waziri katika kufanya strategic policy matters for implementation of the authority. Mimi nadhani hizi ni kazi za wakala. Kwa Bodi ambayo imetajwa, kwa Bodi ambayo ni executive, kwa Bodi yenye maamuzi mimi sidhani kama kazi yake ni kufanya hivyo. Hizo ni kazi zake ambazo zinatakiwa ifanye kama Bodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ukiangalia (j) inasema Bodi itamshauri Waziri. Naomba niisome kwa Kiingereza; “Advice the Minister on performance of the management on the set targets and carries out the policy priorities.”
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sidhani kama bodi itakuwa inampelekea Waziri ni kazi ya bodi hii ku-set target zake si kazi ya kumshauri Waziri. Mimi nadhani hizi kazi pengine walioitayarisha hii sheria wangeangalia vizuri, hizo ni kazi zile zilizokuwepo kwenye wakala, kwa sasa hivi ni kazi za Bodi yenyewe wala sio kazi za Waziri, ni za kwake mamlaka ya bodi hiyo iweze kufanya hayo maamuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 9(1) kinatamka kamati za kitaaluma za huduma za sayansi, jinai nakadhalika. Na kifungu hiki kinasema hizi kamati za kitaaluma zitateuliwa na Mheshimiwa Waziri. Sasa huyu Waziri tutamrundikia mambo mangapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilidhani hizi ni kamati za kuisaidia ile mamlaka, kuisaidia ile Bodi; hizi zingekuwa za kufanywa na ile Bodi; ziteue kamati za kuweza kuisaidia, za kitaaluma. Sasa kumpa Waziri mimi naona kama tunamuongezea majukumu mengi sana ambayo ufanisi wake sasa unaweza usiwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 11(2) kinataja kazi ambazo Mkemia Mkuu wa Serikali anatakiwa kuzifanya, ikiwa ni pamoja na kutoa miongozo kwa ajili ya utekelezaji wa sheria hii, kuzuia matumizi mabaya ya kemikali kuzuia vitu mbalimbali vya kikemikali na bidhaa zingine za kikemikali. Sasa mimi nilikuwa nadhanai hayo yote ni majukumu ya bodi. Tunaposema sasa ni majukumu ya huyu Mtendaji Mkuu tunaisahau bodi nadhani kidogo pale panakuwa hapajakaa vizuri. Kwa hiyo, nilikuwa nashauri tuangalie kwamba hayo ni majukumu ambayo ni ya Mtendaji Mkuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 13(1) kinampa tena Waziri kuteua Wakemia wa Serikali badala ya Bodi, mimi nilifikiri kazi zote hizi zingekuwa za Bodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna adhabu ambazo zinatajwa katika vifungu vingi katika hii sheria, mimi nashauri hizi adhabu zote zingehuishwa zikaandikwa katika sehemu moja badala ya kutajwa kila mahali, karibu sehemu sit azote zinataja adhabu hii, adhabu hii na kuna sehemu nyingine inasema wale watu wakifanya uzembe anafungwa miezi sita; adhabu shilingi milioni tano lakini kufungwa miezi sita. Mimi nadhani hizo zianishwe vizuri ziangaliwe ili ziweze kuleta maana halisi hasa iliyokuwa imekusudiwa.
Mheshimiwa Naibu spika, kifungu cha 25 kinataka maabara zote zisajiliwe, maabara ambazo zipo zote zitasajiliwa na mimi nakubaliana, mimi sina matatizo lakini nataka ufafanuzi hapo Mheshimiwa Waziri atakaposimama. Najua kwenye shule za sekondari huku tuna maabara, shule zote za sekondari zina maabara. Taasisi za umma zimetajwa kwamba pamoja na taasisi za mafunzo, lakini nataka nijue hata maabara za sekondari zote zitasajiliwa au itakuwaje? Na imeweka kabisa kwamba lazima kila maabara isajiiwe. Sasa hiyo tungependa tupate labda ufafanuzi kutoka kwa Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kifungu cha 37(1) mpaka (3) kinampa Waziri mwenye dhamana na mamlaka hii kuidhinisha bajeti badala ya Bodi. Ukisoma pale Bodi haijatamkwa kwamba itaidhinisha bajeti hiyo. Sasa nilikuwa nafikiri kazi mojawapo ya bodi ni kupitia mpango kazi, kupitia bajeti ya mamlaka na kuidhinisha na baadye ndipo kuijumlisha katika bajeti kuu. Sasa naona hapa kinasema kwamba bajeti hiyo itaidhinishwa na Waziri, hilo kidogo naona kama halijakaa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 39 na 40 kinazungumzia taarifa iliyokaguliwa ya mamlaka; na kinasema eti mamlaka inatakiwa iwasilishe taarifa mizezi mitatu baada ya mwaka kuisha; na hiyo miezi mitatu hiyo taarifa iwe imekaguliwa. Nadhani hapo tutakuwa tunachanganya. Kwanza kufunga kwenyewe mahesabu ni miezi mitatu mpaka Mkaguzi Mkuu amalize anahitaji miezi mingine kadhaa. Kwa hiyo hivi ilivyoandikwa; na niliona hata jana tulipitisha sheria nyingine imeandikwa hivyo hivyo; mimi nadhani kwamba tungefata uhalisia kabisa kwamba haiwezekani taarifa ikatayarishwa kwa miezi mitatu ikawa imekamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, na hiyo inaendana sambamba kabisa na hata kwenye hili baraza la wanataaluma wa kemia. Kifungu cha 22(2) kwenye Baraza la Wanataaluma pale kuwasilisha taarifa ya ukaguzi miezi mitatu. Mimi siamini kabisa kwamba taarifa ya miezi mitatu itakuwa imekamilika. Nafiki hapa tutakuwa tunaandika halafu mambo hayawezi kutekelezeka. Kwa hiyo, nilikwa nashauri marekebisho haya yafanyike ili kusudi taarifa ije katika wakati ambao tunajua kwamba kweli itakuwa imekamilika na kifungu cha 23 nacho kinasema hivyo hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika zile taarifa ambazo zimeandikwa, taarifa za fedha za mwaka ambazo zinatakiwa kuwasilishwa zimeandikwa pale. Zote zinazohusiana na fedha wametaja. Sasa mimi nilifikiri ni muhimu basi katika zile taarifa iwekwe pia taarifa ya wakurugenzi ya utendaji wa taasisi, yaani tunaita directors report kwa kitaalamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, directors report ndiyo itakayoonesha majukumu makuu ya taasisi, jinsi walivyotekeleza majukumu yao na shughuli zote jinsi ambavyo zimekwenda.
Kwa hiyo, nilikuwa naomba waangalie hilo, waangalie hayo yote na mengine nitayawasilisha nitakapokuwa nawasilisha naunga mkono hoja asante sana.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara na Serikali kwa kujitahidi kutatua changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, hakuna mahali popote amezungumzia Hospitali ya Mkoa mpya wa Songwe. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga au kuimarisha Hospitali ya Wilaya ya Mbozi, yaani Vwawa kwa kuongeza wataalam, vifaa tiba na bajeti ya hospitali ili itoe huduma kama Hospitali ya Rufaa ya Mkoa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni kuhusu mahitaji ya Madaktari na Wahudumu wa Afya katika zahanati, vituo vya afya na Hospitali ya Vwawa. Hivi sasa Mhudumu wa Afya yaani (Nurse) anahudumia ward zaidi ya moja. Zahanati nyingi zimekamilika lakini zimekosa wafanyakazi, bado kufunguliwa. Suala hili linawakatisha tamaa sana wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu ni kuhusu umaliziaji wa majengo ya Vituo vya Afya katika sehemu mbalimbali. Madai ya muda mrefu ya stahili za Madaktari wa Wilaya ya Mbozi hususan Hospitali ya Vwawa kama vile Night Call Allowance, allowance za majukumu na kadhalika, tafadhali naomba yashughulikiwe haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muhimu; naomba maelezo ya kina, nini kinaendelea juu ya ujenzi wa Hospitali ya Mkoa wa Songwe? Hii ningependa majibu ya kina.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kupunguza kodi mbalimbali na kuanzisha utaratibu wa bulk procurement ili kupunguza bei za pembejeo na hasa mbolea, lakini tunaomba isije ikatokea kama mwaka jana bei zilitangazwa lakini ikawa hakuna utekelezaji wowote. Mfumo wa vocha unakiua chama na Serikali mambo yafuatayo ni muhimu kupewa uzito unaostahili:-

(i) Kukuza kilimo; naamini kuwa kilimo kilichopo kwa sasa ni kilimo kidogo cha kupata chakula tu, nchi haiwezi kuendelea kwa kilimo hiki lazima yaanzishwe mashamba makubwa ya kibiashara ambayo yatatoa ajira rasmi kwa watu wengi, yatazalisha kwa tija na kutumia mbegu bora na zana za kisasa yaani commercial farming. Bila kufanya hivyo, tutaendelea kuimba bila mafanikio makubwa, hili linawezekana kama ilivyokuwa siku za nyuma.

(ii) Kufufua kilimo cha kahawa. Kwa miaka mingi zao la kahawa lilikuwa ni kitovu cha mazao ya biashara.

Hata hivyo, zao hili limeporomoka sana kiuzalishaji nchini. Lazima mkakati wa kulifufua zao hili uandaliwe haraka iwezekanavyo.

Sambamba na hilo, Chama cha Wadau wa Kahawa kiliunda TACRI kwa ajili ya kufanya utafiti wa zao la kahawa. Taasisi hii ilipewa majengo na maeneo yaliyokuwa chini ya Serikali. Hata hivyo, hivi sasa taasisi hii inakabiliwa na changamoto kadhaa. Hivyo, ili kuendeleza utafiti, napendekeza Serikali iichukue taasisi hii na kuifanya kama wakala wa Serikali ili kuongeza ufanisi na tija katika utafiti wa zao la kahawa. Zao hili ni muhimu sana kwa maendeleo ya uchumi wetu.

(iii) Suala la Benki ya Kilimo; Benki hii ni muhimu sana kwa maendeleo ya kilimo. Ni vizuri kufungua matawi katika mikoa yenye kilimo sana ili kuwakopesha wakulima wengi, suala hili ni muhimu sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri ambayo naiunga mkono, naomba kuchangia maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Mbozi kuna Mamlaka ya Maji ya Mji wa Vwawa na Mamlaka ya Maji ya Mji Mdogo wa Mlowo. Wakati wa ziara ya Mheshimiwa Waziri wa Maji, aliahidi kuunganisha mamlaka hizi mbili na kuunda mamlaka kubwa itakayoshughulikia kutafuta, kusambaza na kusimamia maji katika miji hiyo ambayo ni sehemu ya Makao Makuu ya Mkoa wa Songwe. Ni lini Wizara itaanza kutekeleza ahadi hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa maji safi na salama katika Mji wa Vwawa. Hivi sasa hakuna maji kabisa Mji wa Vwawa na yaliyopo ni machafu sana kwa sababu hayachujwi kabisa, yanasambazwa kama yalivyo. Bajeti iliyotengwa ni ndogo sana. Naomba Serikali ifanye kila linalowezekana kutuongezea bajeti ya kurekebisha miundombinu ya maji pale Vwawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi ulioandaliwa miaka mingi iliyopita uliotegemewa kusambaza maji katika Vijiji vya Iyula, Idiwili, Ipyana, Idunda, Igale, Luanda, Senjere na Lumbila. Serikali ina mpango gani wa kutekeleza mradi huu?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji wa Lukuhe – Mlangali ambao ungesambazwa vijiji 14 katika Wilaya, baadhi ya fedha ziliwahi kutolewa na zikatumika vibaya. Naomba kupata maelezo ya kina juu ya hatma ya mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Vijiji vya Ihanda na Ipunga pamoja na kata zake, Serikali ilitoa zaidi ya Sh.320,000,000/=, mradi uliokuwa unafadhiliwa na Benki ya Dunia. Fedha hizo hazijulikani zilipo na mpaka leo hakuna maji katika Kata za Ihanda na Ipunga. Naomba tamko la Serikali juu ya mradi huu na hatua zilizochukuliwa dhidi ya fedha hizi. Naomba kupata majibu ili wananchi wa Jimbo la Vwawa na Mkoa wa Songwe waweze kuwa na imani na Serikali yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawasilisha.
MUswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Usajili wa Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu wa mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia katika muswada huu, lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuleta muswada huu muhimu hapa Bungeni, ambao una maslahi mapana ya nchi yetu kwa kweli nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naipongeza Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kuuchambua muswada huu na kuandika ripoti nzuri sana ambayo imewasilishwa leo Bungeni, kwa kweli tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nitumie nafasi hii kuwapongeza wadau mbalimbali ambao wametoa maoni mbalimbali ya namna ya kuboresha muswada huu. Ni kweli kabisa NBAA inafanyakazi kubwa mbili; kazi ya kwanza ni ya udhibiti (regulator) lakini kazi ya pili ni ya kusimamia uendeshaji. Sasa hizi kazi katika maeneo mengi zimetenganishwa na sisi kama Kamati tuliliangalia sana katika suala hili kwamba namna tunavyoweza kutenganisha, lakini kutokana na hali tuliyoiona tukasema sasa hivi hatuwezi kutenganisha, tutaacha kwanza ziendelee kufanyakazi hiyo ifanywe na NBAA lakini baadae vyama vya kitaaluma vijiimarishe ili kusudi viweze kuchukua jukumu lile la usimamizi wa uendeshaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilifikiri ni muhimu ni masuala mahususi kama mawili au matatu ambayo nataka kuchangia; la kwanza ni hili muswada huu ni wa Tanzania Bara, lakini muswada huu kitendo cha kuwa ni wa Tanzania Bara kunaleta complication, kunafanya kwamba wahasibu walioko Zanzibar na wakaguzi wa mahesabu wa Zanzibar wasiweze kutambuliwa na kusajiliwa na NBAA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tulipoliangalia kwa undani na baada ya kushauriana na Serikali, tumeona hii ni changamoto, lakini tukasema kwasababu masuala ya fedha ni ya Muungano basi Serikali ije iangalie huko mbele, waje wafanye marekebisho kupitia marekebisho ya sheria mbalimbali ili huu Muswada uweze pia ku-apply Zanzibar kama wataona inafaa, lakini baada ya consultation na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Kwa hiyo, sisi tukasema kwa sababu sasa hivi kwa hali ilivyo kwa kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haijahusishwa, tukiamua kwamba tuingize iwe ya Muungano tutakuwa tumekiuka taratibu, kwa hiyo tukaona kwamba tutairudisha nyuma. Kwa hiyo tukasema tuende na Muswada kama ulivyo lakini baadae Serikali ione haja ya kwenda kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar waje na marekebisho baada ya mashauriano kusudi sasa wale wenzetu wahasibu walioko Zanzibar, wakaguzi wa mahesabu waliopo Zanzibar waweze sasa kutambuliwa na kusimamiwa.

Kwa sasa hivi ilivyo NBAA wanasimamia wahasibu kutoka Zanzibar kwa makubaliano yaliyoandikwa kwa memorandum. Kwa hiyo, wahasibu kutoka Zanzibar wanasajiliwa na NBAA, wakaguzi wanasajiliwa na wanafanyakazi Tanzania Bara na wanafanya Zanzibar, lakini kwa makubaliano siyo kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, tunafikiri sasa imefika wakati sheria lazima itamke vizuri kabisa kwa uwazi, kwa hiyo hili sisi tunafikiri Serikali italifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine baada ya kuangalia majukumu ya NBAA yanayofanywa tumeona kwamba NBAA ina kazi nyingi sana; kwanza kazi yake ni kuhakikisha inatengeneza standards za kusimamia taaluma ya uhasibu na standards hizi ziko nyingi sana sasa hivi, ziko za biashara, ziko zile za mashirika ya umma na taasisi za umma ambapo wanatengeneza, wanachukua za kimataifa, wanazi-modify wanahakikisha zina-fit katika mazingira yetu, lakini pia wanalojukumu la kusimamia wana taaluma wote; lakini tatu wanalo jukumu la kuhakikisha kwamba wanahakikisha taaluma hii nidhamu na maadili ya taaluma yanazingatiwa katika utekelezaji wa majukumu; lakini zaidi ya hapo wanasimamia katika kutoa elimu na ujuzi kwa wahasibu hawa ili kusudi waweze kupata maarifa ya kutosha na kuweza kutekeleza majukumu yao sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zaidi ya hayo kutoa huduma kwa wanachama mbalimbali, lakini lipo jukumu lingine kubwa wanatakiwa kupitia ubora wa ripoti zote za ukaguzi zilizofanywa na makampuni mbalimbali na wataalamu mbalimbali (Audited Financial Statement). Sasa tunaona haya majukumu yalivyo ni mengi na ni makubwa, wewe mwenyewe ni regulator, halafu wewe mwenyewe ndiyo mwendeshaji na msimamizi, kidogo inakinzana, kwa hiyo, sisi kama Kamati tumeliona hilo na tumeshauri kwamba Serikali ione haja ya kuanzisha taasisi nyingine ambayo itasimamia baadhi ya majukumu oversight board tumependekeza kuwe na oversight board ambayo inaweza ikasimamia ubora wa taarifa za kiukaguzi zitakazokuwa zinafanywa (Audited Review Financial Statement) zile review waka-review na kupitia italeta ubora na tutaweza kufikia viwango vile ambavyo vinatambulikana kimataifa na tukasema NBAA pia inaweza ikashirikiana katika hiyo oversight board na ika-provide hata Sekretariet kiasi kwamba wakaweza kutekeleza majukumu sawasawa. Kwa hiyo, hili tumeona kwamba ni jambo la msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ni suala la utoaji wa elimu, kwa sababu sasa hivi kama ilivyo katika maeneo mengi na wahasibu wengi pamoja na wakaguzi wa mahesabu wengi wanakuwa na taaluma ile ya madarasani wamefaulu mitihani, wanavyo vyeti, lakini ikija kwenye uhalisia wa kufunga mahesabu imekuwa ni changamoto kubwa na hili hasa tatizo ni kubwa zaidi kwenye upande wa taasisi za umma. Serikalini huko ambako unakuta kwamba mtu anapangiwa kaeneo kamoja tu ikija kufunga mahesabu ni tatizo kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa basi sisi tumesema na Kamati imependekeza na Serikali imekubali nashukuru wamekubali karibu mapendekezo mengi ambayo tumeyaleta, kwamba kuwe na ushirikiano wa dhati kati ya vyama vya kitaaluma na NBAA na kwa mara ya kwanza sasa sheria kwa mabadiliko haya kama yalivyokubaliwa japo sijaiona ile schedule of amendment humu ndani, lakini nafikiri tulivyokubaliana na Serikali kuwe sasa na itamke kuwe na mahusiano na ushirikiano na vyama vya kitaaluma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vyama vya kitaaluma kama Chama cha Wahasibu Tanzania (TIA), lakini kimesajiliwa kama ni chama cha hiari, kuna Chama cha Wahasibu Wanawake Tanzania, lakini kuna Chama cha Wahasibu Zanzibar, vyote vinashirikiana. Sasa tukafikiri kwamba ifike mahali sheria hii ivitambue hivyo vyama, washirikiane na NBAA katika kutoa mafunzo na elimu kwa wahasibu wetu na wakaguzi ili wapate weledi wa kutosha na kuweza kutekeleza majikumu yao kama inavyotakiwa na ili nashukuru Serikali imekubali na ninaamini kwamba mambo yatakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna jambo lingine kulikuwa na pendekezo ambalo limeletwa na Serikali kwamba sasa mhasibu yule mkaguzi wa mahesabu akishakagua hesabu anatakiwa achukue ripoti yake apelike NBAA, halafu sisi tukasema kidogo hili lina mvutano kwa sababu linaleta mushikeri kwa sababu huyu yeye ni mkaguzi, amekuwa engaged na client. Sasa kuchukua ripoti ya client kwenda kuipeleka NBAA ina-breach ethics za makubaliano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tukasema hilo lingeangaliwa, lakini baadae tulikubaliana na Serikali tukasema basi kwa sababu sasa hivi tulitaka kwamba kwenye vitabu anayekuwa charged na jukumu ni Bodi ya Wakurugenzi, lakini tukaona kuiweka Bodi ya Wakurugenzi kwenye Muswada wa Usajili wa Wahasibu na Wakaguzi itakinzana na sheria zingine zinazoitambua, kwa mfano Companies Act na sheria zinazozungumzia Bodi ya Wakurugenzi, kwa hiyo, tukaiacha hivyo hivyo tukasema kwamba ibaki kama mapendekezo yalivyo, huyu mkaguzi akishamaliza kukagua Audited Financial Statement copy yake aipeleke kule anaposimamiwa na taaluma ili taaluma kama kukiwa na mushikeri mtu yeyote akitaka kufanya reference anaweza kufanya reference pale, lakini anaweza pia ikapitiwa na kuangaliwa ubora wa hiyo taarifa na wanataaluma wenzake. Kwa hiyo, hilo nafikiri tumelipendekeza na tumeona ni zuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, na niseme kama alivyosema Mheshimiwa Kigwangalla kwamba labda tunakizana kuanza kutengeneza vitabu vingi. Hatuwezi kujenga Taifa ambalo tunatengeneza vitabu viwili/vitatu ambavyo havifanani, kitabu lazima kiwe ni kimoja taarifa zinazokwenda TRA, zinakwenda NBAA, zinazokwenda kokote lazima zifanane ili Taifa ambalo tunasema liwe unatengeneza vitabu vitatu, sijui vingapi hilo litakuwa ni Taifa la ajabu. Kwa hiyo, mimi nafikiri mabadiliko haya tunayokwenda kuyafanya ni mazuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuna pendekezo ili la assets kwamba taasisi yoyote ikiwa na mali zinazofikia thamani ya shilingi milioni 700 basi au kama wana mauzo turnover ya shilingi milioni 500 waajiri mhasibu anayetambuliwa, mimi nafikiri hili ndiyo tumekubaliana. Mapendekezo ya awali yamesharekebishwa ndiyo tumefikia sasa kwa milioni 500 kwenye turnover na milioni 700 kwenye mali za Serikali naamini hiyo itasaidia sana katika kuhakikisha tunaboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja naomba Wabunge tuiunge mkono sheria hii ipite bila tatizo lolote. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata hii nafasi ili na mimi niweze kutoa mchango wangu katika hoja hii iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri aliyoitoa pamoja na mambo yote mazuri ambayo yameandikwa katika kitabu hiki cha bajeti. Kwa kweli hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimefarijika sana na jinsi ambavyo mmefanya uchambuzi wa masuala mbalimbali katika kitabu hiki, lakini pia nimefarijika na nimefurahishwa na jinsi ambavyo mnajiandaa kwenda kutekeleza Sera ya Elimu ya mwaka 2014.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sera hii inataka kwamba tutakapofika mwaka 2020 watoto wetu wote watakaokuwa wanamaliza darasa la saba wataenda sekondari, kwa hiyo, inahitaji matayarisho ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi naomba nijikite katika kuongelea ubora wa elimu. Ubora wa elimu ni neno pana, ubora wa elimu una mambo mengi, tunaangalia miundombinu, walimu watakaotumika katika kufundisha, maabara, vitendea kazi na vitu vinginevyo, vitabu, mitaala na mambo mengine mengi, hayo yote kwa pamoja ndio yanajumuisha ubora wa elimu. Ni nini kimejitokeza? Sasa hivi mitaala yetu mingi haikidhi mahitaji ya soko, kuanzia shule za awali, shule za msingi mpaka vyuo vikuu katika maeneo mengi haikidhi mahitaji ya wahitaji, haikidhi mahitaji yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko sokoni ni aina gani ya ujuzi unahitajika, ni aina gani ya elimu inahitajika, ni aina gani ya maarifa inahitajika, hiyo mitaala yetu lazima izingatie hayo. Kwa sasa hivi hali iliyopo mitaala mingi haizingatii hayo, mitaala yetu hii haiwaandai vijana wetu katika kupata maarifa ya kuweza kujitegemea, ndio maana watu wengi wanamaliza sasa hivi hawawezi kujitegemea. Hapa tuna kazi ya ziada ya kufanya, kama nchi lazima tufanye kazi ya ziada. Nadhani hili linahitaji participation ya wadau wote kushiriki katika kuhakikisha kwamba hii mitaala ambayo inakuwepo inakidhi mahitaji ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kwenye upande wa vitabu, mimi naipongeza Serikali, mmetoa vitabu ambavyo bado vina mapungufu mengi, lakini angalau mmetoa, lakini mmetoa kwa ubaguzi. Utoaji wa elimu kwenye nchi hii siyo wa sekta ya umma peke yake, kutoa elimu lazima kujumuishwe sekta binafsi na wadau mbalimbali. Hivi vitabu mlivyotoa mnapeleka kwenye shule za umma peke yake, sasa shule za watu binafsi zinapata wapi vitabu? Shule zote zinatoa mchango mkubwa katika kuandaa wataalam na wanafunzi wetu. Hivi vitabu chapisheni, wekeni huko, hizo shule zinunue zitatusaidia sana katika kutoa elimu kwa Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nalisema kwa uchungu kwa sababu tarehe 5 Mei niliuliza swali hapa kwamba ni Watanzania wangapi ambao hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu. Takwimu zilizoletwa kwenye lile swali zinaonesha asilimia 22.4 ya Watanzania hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu. Hiyo inatuonesha ni aina gani ya Taifa tunaenda kulijenga kama Watanzania wengi kiasi hicho hawajui kusoma wala kuandika. Tunaingiaje kwenye kujenga uchumi wa viwanda tukiwa na Watanzania wengi hawajui kusoma wala kuandika? Hapa kama nchi lazima tukae chini tutafakari na tuone namna gani tunaweka mikakati ya kuwasaidia Watanzania hawa ambao hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka miaka ya nyuma tulisoma elimu ya watu wazima, ile mikakati iliyokuwepo ilitusaidia. Mimi nafikiri umefika wakati tuweke mikakati kila kijiji lazima kwenye shule zetu zile wale watu wote ambao hawajui kusoma, kuhesabu na kuandika wakafundishwe kwa lazima. Hatuwezi kujenga nchi kwamba eti wataenda wenyewe lazima wakafundishwe kwa lazima, tupate watu wote wanajua kusoma, kuhesabu na kuandika hapo ndiyo tutakwenda kujenga nchi yenye uchumi wa soko la kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye taarifa zetu inaonesha asilimia 80 na kuendelea watoto wetu kwenye shule za sekondari wanapata division four na division zero na hawa baada ya kumaliza wakiwa wamepata matokeo hivyo wanaenda wapi? Wanaenda kuchangiaje katika uchumi wa viwanda? Ndiyo maana tukasema lazima tuimarishe sekta binafsi tujenge vyuo vingi vya VETA viwachukue hawa viwafundishe, viwape ujuzi, viwape maarifa wakafanye kazi zitakazosaidia kufuatana na kiwango cha elimu walichonacho lakini hivi sasa ukisoma hotuba unaona mkakati bado haujatosha katika kujenga hivi vyuo vya ufundi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Jimboni kwangu, Jimbo la Vwawa na hasa Mkoa mzima wa Songwe hakuna Chuo cha VETA. Nilitegemea hapa useme kwamba Mkoa wa Songwe tunakwenda kujenga Chuo cha VETA sijaona na kule kuna Watanzania na shule nyingi. Baadae nitakuja kujenga hoja ya kushika shilingi kama sijapata majibu nini kinaenda kufanyika katika lile Jimbo la Vwawa na hasa Mkoa wa Songwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema hapa na kila siku tunapiga kelele, hivi kwa nini tuendelee tu kupiga kelele? Tumesema mtoto akipata mimba mwache akajifungue, akimaliza arudi kusoma, kuna tatizo gani? Kwani mtu akipata mimba maana yake asisome?

Maana yake aishie tu hapo? Huyo anaenda kujenga Taifa gani? Lazima huyu mtu akijifungua, akalea mtoto kidogo, arudi kusoma, hakuna haja ya kuweka masharti, kuna tatizo gani? Nadhani tufike mahali tuwe serious katika issues ambazo ni serious. Hawa watoto ambao wanaishia katikati lazima tuchukue hatua, watu wote wapate elimu ya msingi ndipo tutajenga Taifa zuri na lenye maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia motisha kwa walimu. Walimu katika maeneo mengi wamekata tamaa, hawawezi kutekeleza hii mitaala, hawawezi kutoa elimu bora wakiwa na frustrations. Mwalimu anaingia darasani anataka kufundisha anasema lakini ana malalamiko, hapana, tujenge mazingira mazuri, mahusiano mazuri katika kuhakikisha walimu wanakuwa na motisha na maslahi na madaraja yao yazingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Jimboni kwangu kuna walimu wengi madaraja yao yalisimamishwa, hawapati haki yoyote. Hebu liangalieni hilo ili angalau mambo yaende vizuri na tuweze kujenga Taifa ambalo ni zuri lenye manufaa na ambalo litatusaidia sisi wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka pia nizungumzie suala la ile Idara ya Kudhibiti Ubora wa Elimu. Ile idara, nimeangalia kwenye bajeti, imepewa shilingi bilioni 30 na kitu hivi lakini katika zile fedha ni za mishahara, fedha za undeshaji ni shilingi bilioni 3.7 lakini kama watapewa, wanaweza wakafanya kazi kidogo. Sasa hivi ile idara haipewi fedha.
Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kutoa mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, naomba niungane na wenzangu kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika Wizara hii, kwa kweli hongereni sana. Pia nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi anayoifanya ambayo tunaiona, nampongeza sana na sisi sote tuko nyuma yake, tutaendelea kumuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nianze kuzungumzia juu ya upimaji wa ardhi. Katika kupima ardhi, ardhi ndiyo mtaji pekee ambao kila mwananchi wa Tanzania, walio wengi, wanaweza kuwa nao. Ardhi ndicho kitu pekee kinachoweza kutukomboa iwe ni wakulima, wajasiriamali, wanawake au vijana, wote tuna kipande cha ardhi. Pamoja na kazi nzuri abayo Mheshimiwa Waziri amekuwa akiifanya, pamoja na kushusha kodi ya premium kutoka asilimia saba kwenda asilimia mbili; ni kazi nzuri, hongereni; lakini hebu tuangalie bajeti ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu tulionao, bajeti ya maendeleo ambayo imekwenda ni asilimia 30 tu, fedha zilizopatikana ni asilimia 30 tu. Hebu tuangalie malengo waliyokuwa nayo. Katika mwaka huu walipanga kwamba wangetoa hatimiliki 400,000, lakini zilizotolewa mpaka tarehe 15, mwezi Mei mwaka huu ni 33,979, sawa na asilimia nane tu ya lengo la mwaka mzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nakuwa na wasiwasi, malengo ni mazuri, nia ni nzuri, tunataka wawekezaji waje hapa kufanya biashara waje kuwekeza, wanawekezaje kwenye ardhi ambayo haijapimwa? Tunainuaje hiyo, tunawasaidiaje wananchi hawa ili waweze kufanya kazi yao vizuri? Hao wawekezaji wakija wanataka kujenga viwanda, ardhi haijapimwa. Nadhani lazima tuwaunge mkono fedha ziende ili wapime, malengo yao yafikie, kinyume cha hapo hatutafika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeangalia miji yetu ilivyo, miji imekuwa ikikua kiholela, nyumba zimekuwa zinajengwa bila mipangilio. Kule Jimboni kwangu Vwawa, Mji wa Vwawa, kuna maeneo yamepangiliwa, kuna maeneo hayajapangiliwa kabisa, maeneo mengi ni squatters, ukienda miji mingi maeneo mengi bado ni squatters.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kupima hayo maeneo tutaendelea kutumia gharama kubwa katika kuendesha nchi hii kwa sababu hata kuwafikia kwenda kutoa huduma hakupo. Sehemu tunazotaka kwenda kujenga huduma za afya, huduma za miundombinu mbalimbali tunashindwa kwa sababu maeneo hayajapimwa. Sasa kasi ya maendeleo ya wananchi ni kubwa ukilinganisha na kasi ya Serikali ya kupima ardhi. Naomba, kama kuna sehemu ya kuwekeza zaidi hili ndilo eneo la kuwekeza, hapo tutakuwa tumepiga dili zuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiwekeza kwenye ardhi uka-plan, ukaipangilia vizuri, migogoro itapungua, yote itapungua. Nyumba zitakuwa nzuri, kodi zitaongezeka, makusanyo yatakuwa ni mazuri, hata nchi nyingi zinategemea makusanyo ya kodi za nyumba, kodi za viwanja. Sasa kama tusipoipa uzito, tutashindwa. Naomba hilo lipewe uzito unaostahili ili nchi yetu iweze kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo napenda Mheshimiwa Waziri anipe majibu; pamoja na kazi nzuri aliyoifanya, mimi ni mdau kule Kigamboni, kule Kigamboni alitangaza Mheshimiwa Waziri, alipoingia tu madarakani; akasema ndani ya mwezi mmoja watapata hati, sasa naona amepewa hela kidogo hati hazijatolewa Kigamboni. Mpaka leo wananchi hawana hati, leo hii bado tunahangaika, tunajiuliza ule mji, ile satellite ipo au haipo na ile ramani Mheshimiwa Waziri ilikuwa nzuri hata mimi mwenyewe niliipenda lakini iko wapi? Hati wananchi hawana, mpaka sasa hivi tunashindwa hata tufanye nini. Naomba, hebu akalifanyie kazi tupate hati, twende kukopa ili tuweze kuwekeza katika maeneo mengine tuinue uchumi wa nchi hii. Mheshimiwa Waziri, nafikiri hilo ni la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya tatu ambayo napenda kuchangia ni kuhusu Shirika la Nyumba. Shirika hili ni kweli linafanya kazi nzuri, limejitahidi sana kuwekeza, limejitahidi sana kujenga nyumba na kuna changamoto kadhaa wanazo. Hata hivyo, nawaomba Shirika la Nyumba, hebu angalieni kwenye Mkoa mpya wa Songwe, kule Jimbo la Vwawa ndiyo mkoa umeanza, tunahitaji ofisi, tunahitaji nyumba nyingi, hamjaanza na maeneo yapo. Hebu njooni muwekeze pale ili wananchi wapate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mazuri sana, kuna viwanja pale Mlowo, kuna Mji wa Ihanda, kuna maeneo mazuri sana yamepimwa mengine, hebu njooni muwekeze ili wananchi wapate nyumba nzuri zitakazofaa ili waishi. Bila kufanya hayo, kwa kweli tutashindwa kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia pia kwenye kitabu hiki cha bajeti, Mheshimiwa Waziri ameandika, ametupa jedwali kubwa ambalo linaonesha Kamati za Halmashauri za Wilaya za Kugawa Ardhi, maeneo mengi amesema hazijateuliwa, kuna tatizo gani Mheshimiwa Waziri? Kuziteua hizo Kamati zigawe ardhi kuna tatizo gani? Hebu walifanyie kazi, wateue hizo Kamati zifanye kazi, ardhi yote igawanywe, itengwe, itumike kwa jinsi tutakavyokuwa tumeipangilia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niseme, ukichukua hii sekta ya ardhi, sekta ya nyumba, duniani kote ina mchango mkubwa sana na isipokuwa properly managed ndiyo huwa inasababisha hata financial crisis dunia nzima. Sasa hebu naomba tuichanganue vizuri, tuifanyie kazi vizuri ili mambo yawe mazuri na maendeleo ya nchi hii yapatikane. Wananchi wale wanahitaji hizo hati ili waweze kuendelea na nina uhakika, Mheshimiwa Waziri na namkaribisha kule kwenye Jimbo langu la Vwawa, hebu aje atutembelee kidogo. Alikuja Mheshimiwa Naibu Waziri nakumbuka, lakini alikuwa na haraka hatukuweza kuzungumza mambo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mengi pale yanatakiwa yapangiliwe. Mkoa wa Songwe ni mpya, ufanane na mambo mapya. Sasa mkoa ni mpya tena uanze kujengwa hovyo hovyo, kila mahali kuwe hovyo hovyo, hiyo kwa kweli inatuchelewesha, inaturudisha nyuma. Namwomba Mheshimiwa Waziri, hebu aje atutembelee, aje tupange, atuelekeze ili tufanye kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vifaa alivyosema Mheshimiwa Waziri vya kupima ardhi, vile alivyosema atavinunua, najua atakuwa labda hajanunua kwa sababu ya bajeti ndogo, hebu waharakishe vinunuliwe hivyo, vigawiwe kwenye halmashauri zetu vikafanye kazi ya kupima na sisi tutasaidia kusimamia kule ili kazi iwe nzuri, nadhani maendeleo yatapatikana katika nchi hii na kila kitu kitawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sipendi kupoteza muda mwingi, naomba kuunga mkono hoja na naomba kuwapongeza kwa kazi nzuri. Ahsanteni sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII : Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru sana kwa Kamati zote mbili kwa kuleta hizi taarifa na hasa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii na michango yote ya Waheshimiwa Wabunge ambayo wameitoa. Kwa sababu ya muda nitakwenda haraka haraka, najaribu kuchangia katika maeneo machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imezungumzia juu ya utunzaji bora wa misitu yetu. Ni kweli kabisa kwamba tumekuwa na changamoto nyingi sana zinazoendana na misitu na kwa ujumla hatuna mamlaka ya kusimamia misitu yetu yote. Sasa hivi utakuta asilimia 35 inasimamiwa na Serikali Kuu, asilimia 45 inasimamiwa na Serikali za Vijiji; Serikali za Mitaa zinasimamia 7% na watu binafsi wanasimamia 7%, general land ni 5% na mengineyo ni 1%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hali ya namna hii na kwa kuwa misitu ni kitu muhimu sana, lazima kweli tuje na mamlaka moja ambayo italeta usimamizi bora wa misitu yetu na ndiyo maana Serikali tunakusudia kwamba sasa hivi tumepitia Sera ya Misitu iliyokuwepo na sasa hivi tuko katika hatua ya mwisho ya kuja na sera mpya ambayo pamoja na mambo mengine tunafikiria kwamba lazima tuwe na mamlaka moja ya kusimamia hifadhi za misitu yetu, ili angalau kuleta manufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo nilitaka nitoe ufafanuzi kidogo, Kamati imezungumzia juu ya migogoro mbalimbali pamoja na Wajumbe mbalimbali pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia sana kuhusiana na migogoro. Ni kweli kabisa kuna migogoro mingi katika maeneo mengi na hasa katika hifadhi zetu. Migogoro hii imesababishwa na mambo machache yafutayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, ni ongezeko la watu. Ongezeko la watu sasa hivi, tuko karibu milioni 52 na zaidi. Wakati tunapata Uhuru tulikuwa milioni tisa tu; ardhi ilikuwa hii hii haijaongezeka. Kwa hiyo, hii imekuwa ni changamotio kubwa na imekuwa pressure katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, kwenye uwekaji wa mipaka yetu katika maeneo mengine mengi Waheshimiwa Wabunge wamedai kwamba kulikuwa hakuna ushirikishwaji. Inawezekana ni kweli, lakini nataka niseme, mambo yaliyogundulika katika hii migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tumegundua kuna vijiji 366 vimepimwa kwenye hifadhi, vimo kwenye hifadhi. Katika Misitu yote iliyopo, vijiji vilivyopo ndani ya misitu viko 228, hifadhi zenye migogoro ziko 191, wakati huo huo hifadhi zetu kama TANAPA kuna migogoro kama 21, TAWA kuna 23, Mali Kale kuna mmoja na migogoro mingine mingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana baada ya kuona kuna migogoro mingi, Serikali ikaamua kwamba tuwe na Kamati ya Kitaifa ambayo inajumuisha Wizara kadhaa kwa ajili ya kuja na ufumbuzi wa migogoro hii yote ambayo imejitokeza katika eneo moja. Kwa sababu, hii migogoro ni mitambuka, haihusu Wizara ya Maliasili peke yake, ni maeneo mengi.

Kwa hiyo, ni matumaini yangu kwamba hii Kamati itakapokamilisha hii taarifa sasa, itakuja na mapendekezo mazuri kabisa ambayo yatapunguza kwa kiwango kikubwa migogoro ambayo ipo katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu ambalo nataka nizungumzie, linahusu masuala ya mapito ya wanyama. Katika mapito ya wanyama, Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia sana. Ni kweli kabisa, hifadhi zetu sasa hivi kwenye maeneo ambayo yalikuwa ni mapito ya wanyama, shoroba, zimevamiwa na wananchi kwa sababu ya ongezeko la watu na shughuli za kibinadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, madhara yake kutokana na uvamizi huo, labda niseme kuanzia Oktoba, 2016 mpaka 2017, ekari zaidi ya 42,562 ziliharibiwa na wanyamapori kwa sababu walikuwa wanataka kupita katika maeneo. Maeneo yamevamiwa, watu wanashughulika na kilimo, kuna mambo mengi yakiendelea pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa matokeo yake ekari kadhaa zimeharibiwa. Watu waliopoteza maisha mwaka mmoja tu 484; mifugo iliyopotea 191, fedha ambazo Wizara tunatakiwa kulipa kama kifuta jasho, siyo kama fidia, kama kifuta jasho ni zaidi ya shilingi milioni 800.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utakuta…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dokta John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua anazochukua kukabiliana na Upotevu wa Mapato ya Serikali katika Sekta ya Madini
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa kupata hii nafasi na nalipongeza Bunge kwa kuja na hili Azimio ambalo ni muhimu sana katika kumpongeza Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwenye macho haambiwi tazama na mwenye masikio lazima asikie. Rais amechukua hatua nyingi, Rais amethubutu kuzuia makinikia yasiende nje, Rais amezuia kusafirisha madini yote nje, hizo ni hatua za dhati kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu hii ni tajiri sana, tuna madini mengi sana labda nizungumzie kwenye Jimbo langu la Vwawa na Mkoa wa Songwe na Mbeya kuna madini mengi. Kwa mfano, kuna niobium pale kwenye Gereza la Songwe ni madini yanayoweza kutumika kutengeneza injini za ndege, ni madini pekee yamegunduliwa yapo Tanzania. Kuna gesi na kila aina ya madini, tuna makaa ya mawe kule Magamba ambayo hayapo yoyote katika Afrika ni makaa bora, tuna makaa ya mawe kule Kiwira, tuna madini ya dhahabu kule Chunya kuna ugunduzi wa kila aina ya madini.

Kwa sababu Botswana mwaka 2006 ilichukua hatua kama hizo na haikushtakiwa. Utajiri ni wa kwetu, madini ni ya kwetu lazima hatua zichukuliwe. Marais waliotangulia walithubutu kuchukua hatua lakini wale wasaidizi wao hawakuwaunga mkono na ndiyo maana sisi tunasema Marais walifanya kazi nzuri lakini watendaji wasaidizi hawakutekeleza majukumu yao, lazima hawa hatua zichukuliwe. Marais walifanya kazi nzuri na Rais huyu wa Awamu ya Tano hatua anazozichukua lazima ziungwe mkono na kila mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashukuru nimeona baadhi ya Wapinzani wanasema ile Miswada mibovu mibovu ambayo ina matatizo iletwe, ni kweli ndiyo tunachosema zile sheria zote mbovu mbovu, mikataba ya kila namna ambayo ina matatizo iletwe hapa Bungeni, tuipitie upya kwa uwazi ili iweze kuleta maendeleo ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hili ni suala la msingi sana ili nchi yetu iweze kunufaika na rasilimali za madini ambazo ni nyingi sana katika nchi hii. Nchi haistahili kuwa maskini kwa utajiri uliopo ambao tumepewa na Mwenyezi Mungu. Tuna almasi, dhahabu, nikel, uranium na kila aina ya madini, kwa nini tuwe maskini? Lazima tukae chini kama watu tuliokwenda shule tuone ni nini cha kufanya ili nchi yetu iweze kufaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Rais na naomba Wabunge wote tumuunge mkono, tupambane ili nchi hii iweze kuleta maendeleo ya kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nichukue nafasi kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri ambayo ameendelea kuifanya na kuingoza nchi yetu ili tuweze kufikia katika uchumi wa kati. Pia naomba nichukue nafsi hii kumpongeza Waziri wa Ujenzi Mawasiliano na Uchukuzi pamoja na Naibu Mawaziri na Viongozi wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda nitazungumza kwa kifupi nitazungumza hoja chache. Waheshimiwa Wabunge katika kutoa michango yao wamechangia katika maeneo mengi, lakini moja ya maeneo ambayo wameyazungumzia kwa kiwango kikubwa ni pamoja na miundombinu ambayo inaenda katika hifadhi zetu, inayokwenda katika vivutia mbalimbali vya utalii nchini kwetu, wengi wametoa malalamiko na wamezungumzia. Naomba nichukue nafasi hii kusema kwamba nchi yetu ukiangalia maliasili tulizonazo, ukiangalia malikale tulizonazo, ukiangalia hifadhi tulizo nazo milima, maziwa na mambo mengine yote lazima kama Serikali tuwekeze vibaya sana katika maeneo haya ili tuweze kuvutia utalii na tuweze kupata mapato ya kutosha yanatokana na utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuona kwamba hii ni sehemu pekee tunayoweza kupata mapato makubwa tumeamua kuweka nguvu kabisa katika kuimarisha miundombinu ambayo inaunganisha vivutio vyetu vya utalii katika maeneo mengi. Ndiyo maana utaona tunajenga viwanja vya ndege tumezungumzia Uwanja wa Ndege wa Iringa, Uwanja wa Ndege wa Chato ambao utafufua utalii katika maeneo yote yale na katika hifadhi zote zinazoonekana Selous na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo lazima Serikali iwekeze katika miundombinu ya barabara tunataka watalii wa nchi hii wanaokuja katika maeneo yetu wawe na uwezo wa kwenda kwa barabara, wawe na uwezo kwenda kwa ndege, wawe na uwezo wa kwenda kwa kutumia reli, wawe na uwezo wa kwenda kwa kutumia boti na vitu vingine vyote kila mtu atajipima uwezo wake yeye mwenyewe. Ndiyo maana Serikali inawekeza katika maeneo haya, uwekezaji wa namna hii tutapata mavuno makubwa sana baada ya miaka miwili/mitatu inayokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hali hiyo ndiyo maana Serikali sasa tumeamua kununua ndege za kutosha, ndege hizi zitafanya kazi kubwa katika kuvutia utalii na kuimarisha utalii wa nchi yetu. Wapo watu wataongea maneno mengi, ndugu zangu utajiri huu tulio nalo mimi naamini kwanza hizi ndege tunazonunua ni chache ukiangalia hali tuliyonayo bado ni chache, tunahitaji nyingi zaidi. Mimi nadhani tungehitaji tuwe na Dream Liner angalau nne kwa pamoja; mbili ziwe zinaenda Marekani zinapishana kuleta watalii moja kwa moja kuja hapa, mbili ziwe zinaenda bara la Asia kuleta watalii moja kwa moja sasa hivi tunayo moja bado hazitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wanazungumzia hii moja/mbili sijui taratibu, taratibu zipi unachozungumzia hapa ni kuwekeza ili tupate mapato ya kutosha yanayotokana na sekta ya utalii na mambo mengine katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Watanzania, naomba Wabunge wenzangu tuyaangalie mambo haya kwa mtazamo mpana ili nchi yetu iweze kusonga mbele tuweze kupata mapato ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia watalii sasahivi walioko kwenye nchi yetu ambao wamekuja kwa mwaka 2016 tulipata watalii 1,284,279 ambao walituletea bilioni 2.1 dola za Marekani, mwaka 2017 tumepata watalii 1,324,143 wametuletea bilioni 2.3 dola za Marekani; bado ukiangalia vivutio tulivyonavyo watalii hawatoshi. Nchi ya Italia peke yake ukichukua lile Jimbo la Platino peke yake lenyewe lina watu laki sita, lakini linapata watalii milioni sita kwa mwaka sisi ukichukua vyote bado hatuna. (Makofi)

Kwa hiyo, ndiyo maana tunasema lazima tuwekeze, hii reli ya kati standard gauge kwetu sisi ni fursa ya utalii, italeta watalii wengi itatusaidia sana. Kwa hiyo, naomba wale wanaozungumzia sijui ATC imepata hasara, siyo wakati huu sasa hivi ndo tunawekeza hatuwezi kuzungumzia hasara leo, baada ya muda tutapata muda wa kutosha wa kuweza kutathaimini na kuona kwamba hasara ipo au haipo sasa hivi ni wakati wa uwekezaj. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja naipongeza sana Serikali.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali, Waziri na watumishi wote kwa kazi nzuri wanazozifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa mchango wangu wa maandishi katika Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora katika maeneo yafuatayo; kwanza mishahara ya watumishi na kupanda madaraja. Kwa muda mrefu sasa Serikali haijaweza kuongeza mishahara kwa watumishi wa umma na kushusha moyo wa kufanya kazi kwa watumishi wengi. Hali ya mfumuko wa bei inaendelea kuathiri maisha ya watumishi wengi. Ili malengo ya Serikali yafikiwe ni muhimu kuangalia uwezekano wa kuongeza mishahara sanjari na mapunjo ya mishahara na madaraja ya baadhi ya watumishi ambao wamefika muda wa kupanda na kupunguza malalamiko ya watumishi wa umma.

Pili ni kuhusu mfumo wa OPRAS nchini; ni wazi kabisa mfumo huu ni muhimu sana kwa maendeleo endelevu, hivyo Serikali ikasimamie na kufanya kazi kwa uwazi na uwajibikaji. Hivi sasa mfumo unaonekana hauna tija kwa kuwa haujasimamiwa vizuri na kutoa matunda tuliyoyatarajia. Ni vizuri iwepo siku ya kutangaza matokeo ya tathimni ya utekelezaji wa mfumo huu kwa mtumishi mmoja mmoja na pia taasisi. Taasisi zifanyike overall performance na kutangazwa matokeo yao hadharani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu ni suala la Serikali mtandao; naipongeza Serikali kwa kuendelea kuimarisha mifumo ya TEHAMA na Serikali mtandao. Lakini kuna haja pia ya kufanya utafiti na tathmini ya mfumo huu unavyofanyakazi ii kupima mafanikio na kubaini changamoto zilizopo ili nchi ipige hatua kubwa.

Nne, mpango wa TASAF; hivi Serikali imefanya tathimini ya mpango huu na kuona haja ya kuendelea na mpango huu? Hivi sasa maeneo mengi wanalipwa watu wasioruhusiwa na walengwa wanabaki nje ya mpango. Naona ipo haja ya kuangalia mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano ni suala la rushwa nchini; sasa hivi rushwa ni kubwa sana katika miradi na zabuni katika maeneo mengi ya nchi yetu. Je, ni mkakati upi hasa ambao umeandaliwa kupunguza rushwa na kujenga nidhamu, uzalendo, uadilifu na uwajibikaji? Katika taasisi nyingi bado hali si shwari kabisa.

Sita ni kuhusu mafunzo kwa viongozi na watumishi wa umma; kwa muda mrefu wa sera ya mafunzo na utekelezaji wake bado ni kitendawili. Mafunzo mpaka sasa yanachukuliwa siyo kitu muhimu. Ni vizuri suala la mafunzo kwa viongozi wa umma, watumishi wa umma lipewe uzito mkubwa. Huko nyuma suala la leadership competence framework iliandaliwa na Chuo cha Utumishi wa Umma lakini hadi leo halijatekelezwa na hakuna mafunzo kwa kuzingatia framework hiyo. Ni vizuri Serikali ikaliangalia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba masuala hayo hapo juu yaangaliwe na kufanyiwa kazi vizuri ili kujenga misingi ya utawala bora na utumishi uliotukuka.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nichukue nafasi hii, kuzipongeza sana Kamati zote mbili kwa kazi nzuri ambayo wamezifanya na kwa ripoti ambazo wamezitoa ambazo zimetoa ufafanuzi na uchambuzi wa kina wa masuala mbalimbali. Inawezekana tukajadili mambo ya msingi na inawezekana wakati mwingine tukaingia kwenye siasa katika mambo ambayo hayastahili siasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu tunachokijadili hapa ni mahesabu ya Kamati hizi mbili, mahesabu yaliyokaguliwa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali; Kamati ya PAC na Kamati ya LAAC na hizi Kamati kwa kawaida ndiyo zinafanya kazi kwa niaba ya Bunge, kwa niaba ya sisi wote hapa, katika kuchambua taarifa mbalimbali zinazohusiana na masuala ya mapato na matumizi ya fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusema tu kidogo kwamba tunapozungumzia suala lolote kuna vitabu vya uhasibu ambavyo ni vya msingi ambavyo ndiyo vinatupa taarifa za kuzichambua. Hivyo vitabu visipoonesha chochote, ukichangia tofauti na hicho utakuwa una jambo lako kichwani. Sasa ukisoma Kanuni za Kimataifa za Utayarishaji wa Mahesabu ya Umma, ambazo ni IPSAS, ambayo tunaizungumzia sasa hivi imekuja na utaraibu kwamba tunatumia Accrual Account System. Pengine nikilisema hili watu wanaweza wasielewi nifafanue, kuna misingi mitatu unaweza ukatumia Accrual Account System, unaweza ukatumia Cash Accounting System, unaweza ukatumia Modified Accrual Account System. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka yote ya nyuma, miaka ya nyuma tulikuwa tunatumia Cash Accounting System ambayo tulikuwa tunalinganisha fedha ulizokusanya na matumizi uliyotumia, basi umemaliza. Unaposema Accrual Accounting System maana yake, mapato unayoiripoti kwenye vitabu ni mapato ambayo unaweza ukawa umepokea cash, unaweza ukawa hujapokea cash, lakini tayari huduma imeshatolewa. Unapozungumzia matumizi, tunayoyasema yanaweza yakawa ni matumizi ambayo tumeshalipa tayari fedha na yanaweza yakawa matumizi ambayo bado hujalipa fedha, lakini tayari unadaiwa unatakiwa ulipe,

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ukiyajua hayo vizuri, utazichambua hizo taarifa vizuri. Taarifa ya kwanza ambayo tunaichambua ni kitabu cha mali na madeni ambacho kinaitwa Statement of Financial Position inaonesha hayo na hili ukielewe hicho uelewe mali zilizopo, uelewe madeni yaliyokuwepo tarehe ile kwa tarehe 30 Juni mwaka 2017, ndiyo maana tunaita as at 30th June.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitabu cha pili cha muhimu ni kitabu cha mapato na matumizi ambayo tunaita Statement of Financial Performance. Katika hili tunaonesha mapato yote, yale tuliyopokea na ambayo bado hatujapokea lakini tunadai, yote tunaonesha. Ndiyo maana kwenye ripoti ile ya awali mlielekezwa kwamba kuna receivables, ambazo maana yake ni mapato ambayo tumeshatoa huduma, lakini bado hatujayapokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hayo kwa mantiki hiyo hayo ukiangalia kwenye exchequer huwezi kuyaona, sitosikia, kwa sababu ni mapato bado hujapokea, ndivyo hivyo kwenye matumizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitabu cha tatu na cha msingi kinaonesha mtiririko wa fedha yaani Cash Flow Statement; sasa ukiunganisha Cash Flow Statement itakavyoonesha balance huko ilingane na kile kitabu cha mali na madeni ile cash and cash equivalent inayokuwa reported pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiendelea kuchambua kuna kitabu cha nne changes in equity; kuna kitabu cha tano kinaitwa Budgetary Performance Report. Budgetary Performance Report ndiyo inatupa taarifa ya bajeti nzima ya Serikali na matumizi yalivyofanyika katika mwaka huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa unapokuja na hoja kwamba kuna trilioni 1.5 imepotea cha kwanza tunakuuliza unatumia kitabu gani ambacho taarifa hizo zipo? Ndiyo maana ukisoma kwenye vitabu vyote hivyo nilivyovisema ukiongeza Directors report, sijui Accounting Officers report, hakuna hayo. Mtu pekee ambaye angeweza kutuambia hayo kwamba kuna matatizo ni CAG. Kwenye ripoti yake alipoileta hakuonesha kama kuna tatizo, haiwezekani CAG ambaye ni Mtaalam ambaye ana wataalam waliobea akaandika eti akaficha trilioni 1.5 haiwezekani, hilo ni ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ya pili, kwenye Kamati ndiyo maana hoja hii tunayoijadili, ni hoja ambayo imetoka kwenye uchambuzi wa mitaani ambao haupo kwenye misingi ya vitabu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mtu anayeelewa ukichukua huu ukurasa wachambua hata hili ripoti ya Kamati inayoongoza na wenyewe wenzetu, ripoti hii kuanzia pale ukurasa wa 21, 22 23 mpaka 24 wameonesha maana ya reconciliation kuanzia mwanzo mpaka mwisho, mmesoma hizi mmezielewa? Inawezekana tunajadili kwa sababu hatujapata tafsiri hizi za figures. Naomba tuwe na muda wa kutosha wa kuchambua kilichoandikwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nafurahia sana ninapoona kwamba CAG hajaonesha, Kamati yenyewe ya kwao haijaonesha, ambayo ndiyo msingi wa majadiliano ya humu Bungeni. Kwa hiyo na maazimio yao waliyoyasema wameonesha waliuliza, je fedha zilipotea? Wakasema hazijapotea, sasa tunapoteza wa nini? Kwa hiyo, hilo naomba, liwe vizuri, lieleweke vizuri na tusitake kupotoshana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka kusema, vitabu vinafungwa tarehe 30 Juni. Baada ya vitabu kufungwa kuna miezi mitatu, miezi mitatu ile maana yake nini? Maana yake kama kuna matumizi mengine yako yuko kama kuna adjustment, mnatakiwa mzifanye, ndiyo maana mnapewa miezi mitatu. Kwa mfano, inawezekana ikawa watu walichukua imprest, imprest hatuzitambui kama matumizi mpaka pale zinapokuwa zimekuwa retired; sasa zile zote zitakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ukija mwezi wa Tisa ukifunga na ukifunga mwezi wa Tisa unapopeleka kwa CAG vile vinaitwa draft financial stastement, draft maana yake nini, maana yake unapompelekea Auditor akienda akakagua kama kuna maeneo yakurekebisha atakwambia karekebishe hiki, usiporekebisha nitakupa qualified opinion, ukirekebisha hakuna hoja; akikwambia fanya hiki, ukafanya, hoja imekwisha, ndiyo maana ya audit.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri kuna haja ya Bunge lako Tukufu kupewa muda wa kutosha na kupatiwa semina ya kutosha ya namna ya kuchambua hivi vitabu, kwa sababu tukiipata hiyo, nadhani hata matatizo ya tofauti zetu hizi yatakuwa yamekwisha. Hata hivyo, nataka kusema tunafanya kazi nzuri, lakini tunahitaji kuwa na uchambuzi wa kisayansi na wa kina ili tuchangie vizuri tuisaidie Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nawashukuru sana na nawapongeza wote. Ahsanteni sana. (Makofi/Vigelegele)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru sana kwa kupewa hii nafasi, na kwa sababu ya muda nitakwenda haraka haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ambayo ameifanya katika kusimamia uchumi wetu, ambapo viashiria vyote vinaonyesha kwamba uchumi wetu unakuwa na unafanya vizuri. Haijawahi tokea katika historia mfumuko wa bei umeshuka mpaka hadi kufikia asilimia 3.0 kwa kweli ni kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ambalo nataka niliseme kidogo ni kwamba tunayo Benki yetu ya Kilimo ambayo inafanya vizuri na pengine hapa labda nitoe ufafanuzi kidogo benki yoyote, kazi ya benki, ni kutafuta fedha mahali ziliko nyingi na kuzipeleka mahali zinapohitajika na fedha hizo zinaweza zikapatikana kwa wenye mitaji, ama kwenye mikopo ama kwa Wawekezaji kwa hiyo, benki yetu ya kilimo, inazo fedha za kutosha, za kuweza kufanya kazi, na kusaidia kilimo. Na kutokana na hilo basi, ndio maana Serikali tuliamua tukaipa, tukaomba iikopeshe Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko fedha za kununua korosho na kwenda kuuza na imetoa fedha zote. Kwa hiyo, naomba niseme fedha za kununua korosho hatujatumia fedha tulizonunulia, fedha zilipatikana kwenye mkopo kutoka Benki ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitoe ufafanuzi, kumekuwa na taarifa za upotoshaji juu ya bei ambayo tumenunulia korosho, wengi wanasema tumenunua kwa shilingi 3,300. Nataka niseme hivi, bei tuliyonunulia sio hiyo, kwenye miaka ya nyuma utaratibu uliokuwepo ilikuwa ukinunua kwa shilingi 3,300 ndio unaanza kutoka gharama mbalimbali, gharama za magunia, gharama za maghala na vitu vinginevyo, ndio ilikuwa bei. Kwa sasa hivi, ile 3,300 ni ile anayolipwa mkulima, ni ile anayolipwa mkulima, kwa hiyo basi maana yake bei ya korosho, tuliyonunulia unaongeza magunia shilingi 62.50 kwa kilo, unaongeza usafiri kutoka kwenye AMCOS kwenda kweye maghala makuu. Unaongeza maghala shilingi, 38 unaongeza gharama za uendeshaji wa ushirika AMCOS shilingi 70 union shilingi 50 na gharama zingine, unaongeza cess ya Halmashauri ukizijumlisha bei yake tuliyonunulia ni zaidi ya shilingi 3,600. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulichokifanya tumelipa vingine na vingine bado, hatujalipa, tutalipa vyote, ukijumlisha na export duty ya shilingi zaidi ni asilimia 15 ya FOB maana yake ni shilingi 560, ukijumlisha utapata ni zaidi ya 4,190,…

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA KILIMO: Kwa hiyo hizi gharama walizokuwa wanasema, naomba niweke hizo rekodi kwa wale wenzangu ambao hesabu zinapigwa hivyo…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo faida…

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukishamaliza sasa kulipa na kuuza, sasa tumeuza hizo tani laki moja tunaendelea kuuza, mwisho baadae tutapata sasa tumeuliza zote kwa shilingi ngapi, gharama yote wadau wanaohusika tumewalipa shilingi ngapi, ndio tutakuja kujua kama tumepata faida shilingi au kiasi gani, sio wakati huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niweke taarifa vizuri na nihakikishe kwamba Serikali tumefanya vizuri kwa kupitia Bodi yetu ya nafaka na mazao mchanganyiko, mpaka hadi juzi, uhakiki uliofanyika ni wa thamani ya bilioni 442.9 malipo yaliyofanyika hatujakopea hata hizo tulizouza bado, tuliofanya ni shilingi bilioni 424.8; wakulima waliolipwa mpaka sasa hivi, ni 390,466.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vyama vya Ushirika ambavyo, vimelipa ni 605 kati ya vyama 606…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Hasunga.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kutumia nafasi hii na mimi niungane na wenzangu kwanza kuzipongeza kamati zote mbili ikiwemo Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Mahmoud Mgimwa, Mbunge wa Mufindi Kaskazini kwa kazi nzuri ambayo wameifanya na ushauri wa kina ambao wametupatia katika Wizara yetu, kwa kweli tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kwamba kilimo ndio uti wa mgongo na tunafurahi kupata michango ya Wabunge wengi ambayo imechangiwa kwa kiwango kikubwa sana; na sisi tunasema kwamba tunapokea michango yote, tutaendelea kuifanyia kazi na baadae tutaona namna tutakavyoweza kutoa majibu hayo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa sekta ya kilimo inachangia kwa kiwango kikubwa sana katika Pato la Taifa. Inachangia takribani asilimia 28.7 katika Pato la Taifa lna pia inachangia asilimia 65 mpaka asilimia 75 ya ajira mbalimbali ambazo watu wameajiriwa. Vilevile inachangia kwa asilimia 66 katika malighafi za viwandani, na pia tunachangia kwa asilimia 100 ya chakula chote na lishe tunachopata katika nchi hii; lakini zaidi ya hapo kilimo kinachangia kwa asilimia 30 ya fedha zote za kigeni.

Mheshimiwa Spika, kufuatana na mazingira yaliyopo tuna uwezo wa kuongeza uwekezaji katika kilimo na kikaweza kutoa mchango mkubwa zaidi kuliko hizi takwimu zilivyo hivi sasa. Kwa hiyo, pamoja na changamoto mbalimbali ambazo zipo lakini ni wajibu wetu sisi sote kuungana kwa pamoja katika kuhakikisha kwamba tunaondoka katika kilimo cha kujikimu kwenda katika kilimo cha kibiashara. Pia tutoke hapo tulipo ili tuweze kuhakikisha kwamba tunaondokana na tija ndogo na tunapata tija kubwa ili mazao mbalimbali yaweze kuzalishwa vya kutosha.

Mheshimiwa Spika, sasa ili tuweze kufikia hapo kuna mahitaji mengi ambayo tunayahitaji na ambayo Serikali imekuwa ikiyafanyia kazi na wajumbe wengi wamechangia katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, nianze na suala la mbegu. Ni kweli kumekuwa na takwimu ambazo zimetolewa na Wabunge mbalimbali juu ya mahitaji ya mbegu. Kama nchi mahitaji ya mbegu kwa sasa hivi ni tani 187,500; na ninaomba takwimu hizi zikae vizuri. Katika hizi tani 187,500, zinazohitajika kwenye nchi, mbegu ambazo zimepatikana kwa msimu huu mwaka huu ni tani 71,207 na kati ya hizo tani 66,033 sawa na asilimia 93 zimezalishwa ndani, hizo zimezalishwa hapahapa ndani, hazikutoka nje.

Mheshimiwa Spika, mbegu zilizotoka nje ya nchi ni tani 5,175, sawa na asilimia saba tu ya mbegu zote zilizopatikana hapa nchini; na hapa mbegu tunazozisema tunaachia mbali zile mbegu kama pingili za mihogo, miwa, chai, korosho, miche ya kahawa, yote hapa hatujayahesabu; ukihesabu na hiyo ambayo ipo zaidi ya milioni 22 maana yake uwezo wa taifa wa kuzalisha mbegu ni zaidi ya asilimia 96. Kwa hiyo, tunachotegemea nje ni kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunachosema sisi katika yale mahitaji ambayo tunayasema, kwa sababu upatikanaji ni tani 71,000 maana yake wananchi wengi bado wanaendelea kutumia mbegu za asili, ndizo zinazotumika, lakini si kwamba zinatoka nje. Lakini tunakubaliana na maoni ya wajumbe kwamba tunahitaji kuwekeza zaidi ili kuhakikisha kwamba mbegu zizalishwe wakati wa kiangazi, tuimarishe skimu zetu kusudi tuweze kupata mbegu za kutosha.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni mahitaji ya mbolea. Ni kweli kabisa mwaka huu mvua imenyesha vizuri sana katika maeneo mengi na mahitaji ya mbolea yameongezeka kwa kiwango kikubwa kwa sababu wananchi wengi wamehamasika katika kulima. Mahitaji ya mbolea ni tani 586,000 kwa mwaka lakini upatikanaji mpaka sasa hivi tunapoongea leo ni tani 454,339 ndizo zimepatikana. Katika hizo zipo mbelea aina ya DAP ambazo ni tani 71,000 na urea tani 121,000.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo kumekuwa kidogo kuna upungufu wa UREA, mbolea zingine zote zipo, UREA ilipungua. Tulichokifanya ni kuhakikisha kwamba tunaagiza. Hivi ninavyoongea kuna tani 43,000 zipo bandarini na tani 222,000 zipo njiani zinakuja. Lengo ni kutaka kuhakikisha kwamba tunakuwa na mbolea ya kutosha ili ziuzwe kama nguo zinavyouzwa hapa nchini. Kwa hiyo, mbolea zitakuwepo za kutosha bila tatizo lolote.

Mheshimiwa Spika, huu upungufu uliojitokeza ni kwa sababu yule ambaye tulimpa zabuni ya ku-supply kwa mtindo ule wa ununuzi wa pamoja alichelewa kuagiza na hivyo akachelewesha kidogo ndiyo maana tukawa na upungufu wa aina moja ya mbolea, lakini zingine zote zinapatikana kwa wingi hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, mahitaji ya viuatilifu ni mengi na kweli Wabunge wamechangia kwa kiwango kikubwa na sisi tunasema ni kweli kabisa tunahitaji viuatilifu vya kila namna, utafiti tutafanya na maeneo mengine yoyote tutayarekebisha.

Mheshimiwa Spika, najua kwa sababu ya muda haukuweza kutosha, tungeweza kujibu maswali yote lakini tutaweza kuwajibu Wabunge na tutaleta mbele ya Bunge lako Tukufu, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya pamoja ya ziada ya Nagoya – Kuala Lumpur kuhusu Uwajibikaji Kisheria na Fidia kwa Madhara yanayoweza kutokea kutokana na matumizi ya Bioteknolojia ya Kisasa katika Kutekeleza Itifaki ya Cartagena (Nagoya – Kuala Lumpur Supplementary Protocol on Liability and Redress on Cartagena Protocol on Biosafety) pamoja na Azimio la Kuridhia Itifaki ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika kuhusu Kulinda Haki Miliki za Wagunduzi wa aina mpya za Mbegu za Mimea. (Protocal for Protection of New Varieties of Plants (Plant Breeder’s Rights) in The Southern African Development Community – SADC) pamoja na Azimio la Kuridhia Mkataba wa Marrakesh wa mwaka 2013 unaowezesha upatikanaji wa kazi zilizochapishwa kwa watu wasioona, wenye uoni hafifu au ulemavu unaomfanya mtu kushindwa kusoma (The Marrakesh Treaty to Facilitate Access to Published Work For Persons Who Are Blind, Visually Impaired or Otherwise Print Disabled)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naomba nichukue nafasi hii kwanza kukushukuru wewe mwenye binafsi kwa kutupa nafasi. Pia nashukuru Kamati ya Kilimo Maji na Mifugo kwa michango mizuri ambayo wametoa kwa namna ambavyo wameishauri Serikali na sisi tunasema kwamba ushauri wao wote tumeupokea, tutaufanyia kazi ili tuweze kutekeleza vizuri itifaki hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa SADC. Kwa kweli tunampongeza sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuridhia itifaki hii ya maendeleo za nchi za Kusini mwa Afrika, inatupa heshima kubwa kwamba Mwenyekiti wetu sasa atakuwa na nafasi nzuri ya kuweza kutekeleza majukumu yale yote ambapo amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Nchi za SADC. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge tuunge mkono itifaki hii kwa sababu ina manufaa makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imetoa maoni mengi kuhusu uwekezaji kwenye utafiti na wengi wameshauri kwamba Serikali iangalie uwezekano wa kuwekeza asilimia moja kwenye mapato ghafi ya Taifa. Ni kweli wazo ni zuri na wengi wameshauri hivyo, tunapokea, lakini nataka niseme tu kwamba uwekezaji kwenye utafiti tunaouzungumzia ni utafiti kwa ujumla, siyo kwenye kilimo peke yake. One percent kutoka kwenye GDP ni kwenye utafiti wote katika Wizara nzima, iwe kwenye elimu iwe kwenye kilimo na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo, maana yake ukichukuwa kwa mfano sasa hivi pato la Taifa ambalo ni takribani zaidi ya Dola za Marekani bilioni 54, maana yake tunahitaji karibu almost trilioni moja kwa ajili ya uwekezaji. Ni wazo zuri, nasi Serikali tunalipokea, lakini wakati wa kupanga vipaumbele, tunaangalia kwa sababu ya mapato kidogo yanayokuwepo, vipaumbele ni nini? Tuwekeze kiasi gani? Kwa hiyo, hili tunalichukuwa, tunaendelea kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya utafiti, inatoka kwenye vyazo vya ndani, inaweza ikatoka kwa Washirika wa Maendeleo, inaweza ikatoka kwa watu binafsi. Sisi kama Serikali kwa mfano upande wa kilimo, mwaka huu tumetenga zaidi ya shilingi bilioni nane kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunafanya utafiti wa mbegu; na hizi hela tutahakikisha kwa kweli TARI wanafanya vizuri katika kufanikisha utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi Wagunduzi wetu wa mbegu wamefanya vizuri sana. Kwa mfano, katika Afrika sina uhakika kama kuna taasisi kama TARI kule Naliendele, kazi ambayo wameifanya na ugunduzi ambao wameufanya na mbegu ambazo zimegundulika, sina uhakika kwenye zao la korosho kama kuna taasisi hapa Afrika ambayo imefanya kama vile; na mbegu zetu sasa hivi zinatumika katika nchi nyingi hapa Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuridhia itifaki hii, maana yake manufaa ya mbegu zetu ambazo zinatumika sasa hivi Zambia na nchi nyingine, tutakuwa na uwezo sasa wa kupata angalau mrahaba unaotokana na ugunduzi huu. Kwa hiyo, nataka kusema kwamba mambo ni mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo kazi ya kufanya mapitio. Sasa hivi tunapitia Sera yetu ya Kilimo ya Mwaka 2013, pia tutakuja na sheria mpya ambayo itakuwa ni jumuifu, ambayo itarekebisha vikwazo vyote ambavyo vitafanya itifaki hii ishindwe kutekelezeka. Kwa hiyo, tutarekebisha kama tulivyoshauriwa na Waheshimiwa Wabunge na Kamati, haya yote tutayazingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge, pamoja na Mheshimiwa Haonga wamechangia sana namna ya kuboresha mbegu, nami nakubaliana na suala la kubadilishwa mbegu za asili. Mbegu za asili ndiyo zimetufikisha hapa, nasi tutakuja sasa hivi na sheria nyingine kwa ajili ya kulinda hizi mbege za asili. Kwa sababu ili uje na mbegu nyingine za kisasa, ni lazima hata mbegu ya asili uitambue; na utakapokuwa una-cross, unaunganisha, basi zote hizi tunataka tuwatambue na tuhakikishe tunalinda kwa maslahi mapana ya Taifa letu. Nina uhakika kama haya tutayatekeleza, mambo yatakwenda vizuri sana. Kwa hiyo, nilihakikishie Bunge hili kwamba itifaki hii itakuwa na manufaa makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, faida ni nyingi tumeshazisema, kwa sababu ya muda hatutaweza kusema mengi, lakini nawaomba Waheshimiwa Wabunge wote kwa pamoja, turidhie Itifaki hii ya Ugunduzi wa Mbegu Mpya za Mimea ili ziwe na manufaa na wagunduzi wetu wapate kuwa na motisha ya kuendelea na ugunduzi na kufanya utafiti wa kila namna; nami nina uhakika mkisharidhia, wagunduzi wengi au watafiti wengi wataenda kuwekeza kule kwa sababu wana uhakika sasa wakiwekeza watapata faida na watapata mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipatia hii nafasi ili nami niweze kuchangia katika mjadala huu unaondelea. Kwanza nianze kwa kukipongeza Chama Cha Mapinduzi kwa ushindi mkubwa uliopatikana katika uchaguzi mkuu, lakini pia naomba nimpongeze sana Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi sana katika awamu hii ukilinganisha na mahali tulikotoka, lakini pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Vwawa kwa kunichagua na kunifanya kwamba niwe Mbunge kwa awamu ya pili, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunachangia hotuba ya Rais na ninaona hapa kuna hotuba ziko mbili, ya mwaka 2015 na ya mwaka 2020. Na mimi naamini lengo la hotuba zote mbili ni kutupa mwelekeo kwamba tulikotoka tumetoka wapi, tumefika wapi, tunataka twende wapi.

Mheshimiwa Spika, Baba wa Taifa aliwahi kutuambia kwamba ili nchi yoyote iweze kuendelea inahitaji vitu vine, tunahitaji ardhi, watu, siasa safi na tunahitaji uongozi bora katika hivi vitu vyote tumepata mafanikio makubwa. Cha kwanza ardhi tunayo ya kutosha, watu tunao, lakini siasa safi tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao uongozi tumekuwa na tatizo dogo kwenye uongozi na tunaona kabisa nchi yoyote inayotaka kuendelea duniani uongozi imara ni msingi mkubwa sana katika kulifanya Taifa lolote lifikie malengo yake. Na kwa hatua hiyo, ukichukua hotuba ya Rais yam waka 2015 aliyoitoa mambo aliyoyafanya na tukiona matokeo yake sasahivi, labda kwa sababu ya muda nitasema tu machache.

Mheshimiwa Spika, la kwanza kwa kuonesha umahiri wa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, la kwanza jambo lililoshindikana kwa miaka yote ya Serikali zote zilizotangulia pamoja na kwamba, kila Serikali ilifanya mambo makubwa, lakini jambo lililoshindikana la kuhamishia Serikali Dodoma limewezekana. Hiyo inapima ubora wa kiongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili alilolifanya Rais Magufuli ni kuikokota nchi kutoka kwenye nchi maskini na kuifikisha kuwa nchi ya kipato cha kati. Hili sio jambo la kubeza, ni jambo kubwa ambalo limefanyika, ni jambo kubwa ambalo viongozi wote wanastahili kupongezwa likiwemo Bunge la Kumi na Moja kwa kazi kubwa ya kuisaidia nchi kutoka tulikotoka mpaka tumeiingiza kuwa nchi ya kipato cha kati. Sasa tumekuwa ni nchi ya kipato cha kati kwenye ile lower boundary. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ukiisoma ile hotuba ina mambo mengi, kwa sababu ya muda siwezi kusema, lakini jambo la tatu ni miradi mikubwa aliyoweza kuitekeleza ambayo Serikali ya Awamu ya Tano imetekeleza ambayo imebaki kama alama. Ukichukua mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa ambao unaendelea sasa hivi, mkoloni alijenga reli ya kati, tulipopata uhuru tumejenga reli ya TAZARA, sasa tunajenga SGR kwa hela yetu. Hili ni jambo la kujipongeza na ni maendeleo makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi wa kujenga bwawa la umeme, tunajenga kwa fedha zetu. Tumenunua ndege, tunajenga viwanda, barabara, kila aiina ya mafanikio. Haya yote ndio yanapima utekelezaji wa hotuba aliyoitoa Rais mwaka 2015. Mwaka 2020 Rais anatuambia nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda ni quote ukurasa ule wa 26. Anasema, “mbali na hatua hizo kwa lengo la kukuza uchumi, kupambana na umaskini na pia kukabiliana na tatizo la ukosefu wa ajira tunakusudia kwenye miaka mitano ijayo kuweka mkazo mkubwa katika kukuza sekta kuu za uchumi na uzalishaji, hususan, kilimo, ufugaji, uvuvi, viwanda, madini, biashara na utalii.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana yake nini? Hotuba ya Rais aliyoitoa ya awamu ya pili inatupa muelekeo wa Serikali ya Awamu ya Tano kwa kipindi cha pili. Na hii kama kweli tukiweka nguvu tukawekeza kwenye sekta za uzalishaji za kukuza uchumi ni wazi kabisa miaka mitano itakapokwisha tutakuwa tumefikia sasa kwenda kuwa nchi ya kipato cha kati cha uwanda wa juu. Na hili linawezekana kama Bunge litaweka targets na malengo thabiti ya kuisimamia Serikali na kuishauri Serikali. Na ninaamini haya yanawezekana kwa uongozi wako na kwa uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mungu awabariki. Ahsanteni, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona na nashukuru kwa kunipatia nafasi.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza nianze kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maono mazuri na hotuba nzuri aliyoitoa ambayo imetoa matumaini makubwa sana kwa Watanzania na kuonyesha mambo mbalimbali ambayo tunatakiwa tuyasimamie katika kujenga uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, lakini pili nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuja na Mpango huu wa Miaka Mitano ambao kwakweli umekuja na majibu mazuri ya mambo mengi ambayo tunayahitaji kama nchi, na hasa nimepitia yale malengo yalivyoandikwa, shahaba za utendaji tulivyoziweka, basi nafikiri ni Mpango mzuri kama tukiusimamia unaweza ukatufikisha mahali pazuri.

Mheshimiwa Spika, Mpango wowote ambao tunakuja nao lazima ujibu masuala mazito ya kitaifa ambayo tunaona kama Taifa ni changamoto; na moja ya jambo la kwanza ambalo ni changamoto sasa hivi ni umaskini ulio mkubwa kwa Watanzania walio wengi. Kwa hiyo katika mpango huu lazima tueleze namna gani tunakwenda kutatua umaskini huu ili Watanzania hawa sasa wakuwe na wawe ni wakulima wakubwa, wawe ni wafanyabiashara wazuri, wawe ni walipa kodi na ina maana tutakuwa tumeongeza idadi ya walipa kodi.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili, tunalo tatizo kubwa la kitaifa la ajira, ajira isiyo rasmi na ajira ambazo ni rasmi. Kwa Tanzania sasa hivi watu tulio wengi uchumi wetu ni uchumi ambao sio uchumi rasmi. Kama nchi hii haitupeleki pazuri. Lazima tuchukue hatua za dhati kuhakikisha tunajenga uchumi ulio rasmi ili tupate uchumi ambao ni imara na shindani.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ni kuangalia dhana, teknolojia na tija katika nchi yetu, hili bado ni tatizo kubwa; hatuwezi kufika bila kuchukua hatua zinazostahili. Lakini la mwisho ni uongozi bora wenye maono na Rasilimali watu; hili ni eneo ambalo ni muhimu sana. Sasa nimeangalia katika documents zote tatu zinazotakiwa ziuhishwe ili zote zijibu haya tunayoyasema.

Mheshimiwa Spika, cha kwanza ni Dira ya Taifa, dira yetu ya miaka 25 kuanzia 2000 mpaka 2025. Dira ile ina mambo matano ya muhimu ambayo tunatakiwa kuyafanya; na tutakapofika mwaka 2025, tunatakiwa twende tukapime, je Watanzania tumefikia kuwa na kipato cha dola 3000? na kama hatujafikia ni kwa nini? Hili lazima tuliangalie.

Mheshimiwa Spika, nimeangalia Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Ilani ya Chama cha Mapinduzi ina vipaumbele sita na vimeandikwa vizuri sana. Vipaumbele vile kwasababu ya muda sitaweza kuvisema, ningetamani niviseme. Lakini unakwenda sasa kwenye mpango, mpango umekuja na vipaumbele vitano. Sasa tunaangalia ilani inasemaje, dira inasemaje na mpango unasemaje katika kutekeleza hivi vipaumbele.Nadhani tuna haja ya kuviangalia vizuri na tuhakikishe vyote vinatupeleka katika kwenda kufikia malengo tuliyokusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu walipa kodi wa kwetu wa nchi hii. Sasa hivi biashara nyingi Tanzania ni zile za wafanyabiashara wa chini na wale wa kati ndio walio wengi. Tunafanyaje sasa kuwasaidia hao wafanyabiashara wadogo wadogo? Kama vile boda boda, mama ntilie na wakulima watoke kwenye hizi biashara ndogo ndogo waende kwenye biashara kubwa ambazo wataweza hata kulipa kodi na wakachangia kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili ni kuhusu wakulima wetu. Kilimo chetu hiki hatutaweza kutoka kama hatutaweza kuwahudumia wakulima wetu kama walivyo.

Mheshimiwa Spika, tatu wafugaji, lakini nne ni wavuvi na mwisho ni wachimba madini. Hivi vyote ni vitu muhimu sana, na ndiyo maana Ilani yetu, Mpango wetu huu wa Miaka Mitano useme ni namna gani tunaenda kufanya katika kuhakikisha sekta za uzalishaji zinaongeza uzalishaji. Mkazo katika huu mpango lazima uwe hizi sekta za uzalishaji, sekta za uzalishaji ndizo zitaleta fedha zitakazo kwenda kutumika katika sekta za huduma za jamii na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hasa sekta za uzalishaji ziko kama hivi zifuatazo; tuna kilimo, mifungo, uvuvi, madini, Utalii na Mazingira, Viwanda na Biashara. Sasa, mpango unatuambia nini katika kufanya haya? Tumeweka mikakati gani katika namna ya kwenda kuyatumia ili haya sasa yote yatupeleke kuhakikisha kwamba ikifika 2025 tumeshaingia kuwa nchi ya kipato cha kati lakini malengo yetu ni kuhakikisha nchi inakuwa ya kipato cha kati ambapo kila Mtanzania pato la kawaida iwe ni zaidi ya dola 3000? Sasa hili ndilo lengo tulilojiwekea miaka 2000 iliyopita.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi ninataka kusema tunatengenezaje hizi ajira? Tunawaondoaje hawa Watanzania hapa tulipo? Tunajengeje viwanda? Hii ya kuandika tutaandika vizuri sana na nimeona mipango ni mizuri, lakini tunajengaje viwanda kama ajenda ya kitaifa? Tuna mfuko wa kwenda kujenga? Na kama haya yahawezekani basi maana yake hatutaweza kuja kuyafikia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Hasunga.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru sana kwa kunipatia hii nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu. Jambo la kwanza naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri ambayo ameitoa. Hotuba ambayo imekuwa ni pana, imekwenda kwa mapana na uwanda mpana sana. Karibu kila kitu amekizungumza vizuri sana. Kwa kweli tunampa hongera. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, nchi yoyote, kiongozi yoyote anayekuwepo katika taasisi au kwenye nchi lazima awe na maono. Kuwa na maono maana yake ni kuwa na dira na dira hiyo ukiwa nayo lazima uwe na uwezo wa ku- share na wengine wote na wenzako waweze kuiimba hiyo dira na hao waliofanya hivyo ndiyo walioweza kufanikiwa kwa kiwango kikubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, baba yetu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, aliyekuwa Rais wetu alikuwa na maono makubwa, alikuwa na mtazamo na dira kubwa. Ile dira aliweza ku-share na wenzake na ndiyo maana nataka niseme Magufuli alikuwa akisema, wa pili mama yetu Samia Suluhu Hassan, yeye alikuwa anaenda kutekeleza na kufuatilia utekelezaji. Msimamizi wa Serikali, Kassim Majaliwa Majaliwa yeye ana wahi site, ikishasemwa tu anawahi kwenye utekelezaji na ninayo mifano michache ninayoweza kusema. Nakumbuka wakati ule hayati Dkt. Magufuli aliposema atahakikisha Serikali yake inahamia Dodoma, alipotamka tu lile neno niliona wale viongozi walivyotekeleza yale maono. Wa kwanza alikuwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu, akasema ndani ya miezi mitatu nahamia Dodoma na kweli akafanya hivyo. Makamu wa Rais kahamia Dodoma maana yake ile dira ilikuwa shared. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, alipotamka kwamba tunatakiwa tujenge bwawa kubwa la kuzalisha umeme, walichokifanya nilimwona Waziri Mkuu ameenda site kwenda kuangalia mahali ambapo daraja litajengwa. Ukiangalia Makamu wa Rais ameenda huko, kwa hiyo mambo yote walikuwa wana-share na ndiyo maana hatuna wasiwasi na miradi yote ambayo imeanzishwa katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Tano kwamba yote itatekelezwa vizuri kwa sababu viongozi waliokuwa wanayaimba hayo ndiyo hao ambao bado wako madarakani. Kwa hiyo hatuna wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichukue nafasi hii kuwapongeza. Kuna watu wana wasiwasi kwamba mradi wa SGR, eti hautakamilika, nani anasema? Ule mradi ni wa muhimu, reli ya Standard Gauge aliianzisha Dkt. Magufuli, viongozi wetu wakatufundisha, Bunge likapitisha fedha, leo hii usikamilike, tutakuwa kwa kweli hatujaitendea haki nchi hii. Mradi wa Bwawa la kuzalisha umeme la Nyerere, walipolisema tulipitisha hapa Bungeni, lile bwawa lazima likamilike na litaleta maendeleo makubwa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sio hiyo tu, barabara nyingi zimejengwa za juu, za chini; madaraja tumeona, viwanja vya ndege vimejengwa, ndege zimenunuliwa, nani leo hii anaweza akaiambia hii nchi kama wewe hujaweza kupanda hata hiyo ndege una tatizo lako binafsi, lakini ndege zipo. Hizi zote ndiyo zimebeba uchumi wa nchi yetu. Hawakuishia hapo, wameenda kwenye afya, elimu, maji na kadhalika. Tumeenda mpaka kwenye kujitosheleza kwa chakula. Nchi hii tulikuwa hatujitoshelezi kwa chakula, alipoingia Hayati Dkt. Magufuli akasema kokote kutakakokuwa na njaa, huyo Mkuu wa Mkoa na Wilaya watanikoma na kweli hatujawahi kupata njaa mpaka sasa hivi na ndiyo maana uzalishaji uko wa kutosha. Wananchi sasa hivi wanacholalamikia ni soko, wapi wauze mazao yao. Hilo ndiyo limekuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninachotaka kusema walifanya kazi kubwa, alifanya kazi nzuri na mimi nasema tutaendelea. Miradi ya maji pale Vwawa alitoa fedha mradi wa maji, maji pale bado pana tatizo. Fedha zimekwenda, mradi umetekelezwa lakini maji bado hayatoki. Tuliahidi kwamba hospitali ya rufaa itajengwa pale Vwawa, Ilembo, imeletwa fedha imejengwa ilitakiwa ianze mwezi Novemba mpaka sasa hivi haijaanza. Naomba watendaji waende wakashughulikie hayo kwa sababu ni ahadi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Sasanda kulikuwa na kambi ya kuendeleza vijana. Kambi ile ni muhimu ikaendelezwa ili vijana wa nchi hii waende sasa wakajifunze maarifa, uzalendo na miradi mbalimbali ili waweze kuchangia katika maendeleo ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalo soko la mazao. Mheshimiwa Rais aliyeondoka alituahidi, yote hayo lazima tuyakamilishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka nilichangie ni upande wa watumishi. Mahali popote ili uweze kukamilisha kitu cha kwanza ni watumishi na zamani tulikuwa tunasema mteja ni mfalme, siku hizi mteja ni namna mbili, wa kwanza ni mtumishi. Mtumishi yule ukim-treat vizuri ndiyo atakayefanya hata wateja waongezeke na wapatikane na waende vizuri. Kwa hiyo basi, kwa kuwa tumetekeleza miradi mikubwa na tunaendelea kuitekeleza na ahadi na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ilikuwa ni kwamba sasa tunaingia kwenda kuhakikisha watumishi wetu wanapata maslahi mazuri ili wale ambao madaraja yalikuwa hayajapandishwa, zile promotion ambazo zilikuwa hazijafanyika, mishahara ambayo ilikuwa haijaongezeka, basi sasa ni kipindi naiomba Serikali yetu sasa iwatazame hawa watumishi wa Serikali waweze kuongezewa ili waishi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sio hao tu, watumishi wa Sekta Binafsi. Serikali ilipanga vima vya chini vya mishahara ya Sekta Binafsi zote, vima vya chini vile waajiri wengi hawajavizingatia. Ningeomba ili Watanzania wawe na maisha mazuri ili wananchi wawe na maisha mazuri waweze kuchangia basi naomba Serikali ikaangalie maeneo hayo. Ninachotaka kusema, miradi mikubwa hii ya vielelezo, ndiyo imebeba uchumi. Uchumi wa nchi yetu umefika kuwa ya kipato cha kati kwa sababu ya hii miradi ya vielelezo na miradi hii tusimame pamoja isitokee hata mmoja wetu mara anaanza kubeza, mara mwingine anaanza kusema huu mradi tuuache tutakuwa kwa kweli hatujaitendea haki nchi hii. Miradi ya umeme, umeme kule wanahitaji, una shida sana kwenye Mkoa wa Songwe. Kule vijiji vyote ambavyo havijapata vinahitaji umeme, lakini hata mahali ambapo uko bado kuna changamoto unakatikakatika. Tunaiomba Serikali ikasimamie, ikatekeleze ahadi zake ili umeme ule upatikane. Zile barabara ambazo ziliahidiwa tulifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ninalotaka kusema ni kuhusu Mradi wa Chuma wa Liganga, huu lazima tuutekeleze. Ni mradi mpya lazima tuutekeleze, tutenge fedha, tukautekeleze huo, tukipata chuma chetu tutaweza kujenga viwanda imara, tutaweza kupata malighafi hapa hapa nchini na tukiwa na umeme wetu ndiyo maendeleo makubwa yataweza kuwepo. Bila kufanya hivyo, tutashindwa kwa kweli kuweza kufanikiwa kama nchi na kufikia yale malengo tuliyojipangia kwamba ifikapo mwaka 2020 tutafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naamini kwa jinsi tulivyojipanga na kwa jinsi Bunge hili linavyofanya kazi nzuri na kwa Watanzania ambavyo sasa tunataka kuona nchi yetu inaendelea, naamini tutaweza kufika kuwa nchi ya kipato cha kati cha uwanda wa juu na hayo yanawezekana kwa kufanya kazi kama timu, kwa kushirikiana, tuondoe ubaguzi, tuondoe utengano, tuwe kitu kimoja. Mungu awabariki. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia hii nafasi. Jambo la kwanza, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu kwa ujumla kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kwa sababu upatikanaji wa maji safi na salama ni moja ya vipaumbele; na ni kipaumbele cha nne kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 – 2025. Kwa hiyo, nampongeza sana kwa hotuba nzuri ambayo ameitoa na mwelekeo ambao ametupatia kwa kweli unatupa matumaini makubwa.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, napenda kushauri; kwa muda mrefu tumekuwa tunapitisha bajeti kwa figures kubwa sana, lakini upatikanaji wa hizo fedha kiuhalisia umekuwa ni mdogo sana. Ukiangalia katika miaka yote ambayo tumepitisha bajeti, ukija kusoma uhalisia wa fedha ambazo zimepatikana kwenda kutekeleza miradi ni kidogo sana.

Mheshimiwa Spika, hata sasa hivi nimepitia ripoti ya Kamati nikaangalia ni kiasi gani cha fedha ambazo zimepatikana? Utakuta wanasema fedha zilizopatikana mpaka sasa hivi na ambazo zimekwenda ni shilingi bilioni 376.4, sawa na asilimia 53.3. Kwa hiyo, hii inatia wasiwasi kidogo. Miradi tunaipanga vizuri, kazi tunazipanga vizuri, lakini fedha zisipokwenda inakuwa ni vigumu sana kuweza kutekeleza hiyo miradi ambayo tumekusudia.

Mheshimiwa Spika, kwenye Jimbo la Vwawa kuna mradi mkubwa pale Makao Makuu ya Vwawa ambao ulikuwa unatekelezwa, tulipata shilingi bilioni 1,500 kutoka kwenye chanzo cha Mantengu kwa ajili ya kusambaza maji katika Mji wa Vwawa. Mradi huu ulizinduliwa na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano na alipokuja kuzindua akatoa tena fedha shilingi milioni 100 ili kuhakikisha kwamba usambazaji wa maji unaenea katika ule Mji wa Vwawa.

Mheshimiwa Spika, pia Waziri aliyekuwepo alitoa fedha kwa ajili ya uchimbaji wa visima vitatu virefu ili visaidie katika kuongeza mtandao wa upatikanaji wa maji. Cha kushangaza, mpaka leo bado kuna shida kubwa ya maji katika Mji wa Vwawa na yale maji hayajasambazwa, zile fedha sielewi zimefanya nini? Vile visima toka vimechimbwa zaidi ya miaka karibu mitatu bado havijaanza kufanya kazi kwa kisingizio kwamba hakuna fedha za kuunganisha ili viweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, sasa hilo, nakuomba Mheshimiwa Waziri, pamoja na kazi nzuri anayoifanya, basi hebu akalimulike hilo ili vile visima ambavyo vimeshatumia fedha, basi vikafanye kazi ili wananchi waweze kunufaika na upatikanaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilitaka kusema, kuna mradi wa maji wa pale Kata ya Ihanda, ni wa muda mrefu sana, umekuwa na shida, ambao ungesambazwa katika vijiji mbalimbali pale Ihanda. Ulikuwa na matatizo. Mmetoa shilingi milioni 200, bado maji hayajapatikana. Tumechimba kisima, mpaka sasa hivi bado ni shida. Hebu naomba mkalifuatilie mlifanyie kazi ili wananchi wa Kata ya Ihanda na vijiji vyote vinavyozunguka eneo lile viweze kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, zaidi ya hapo, kuna Kata ya Ipunga pale, kuna Vijiji vya Mpera, Ipunga yenyewe, vinahitaji maji. Vinaweza kupata maji kutoka kwenye mto kwa njia ya mserereko, lakini mpaka sasa hivi bado kumekuwa na changamoto ule mradi haujaweza kutekelezwa. Hiyo imekuwa ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Spika, kuna Vijiji cha Msiya, Weruwan, Iganduka na maeneo mengine ya Isararo yanayozunguka. Pale tungeweza kupata maji ambayo yangetoka; kuna mradi mkubwa ambao uliwahi kusanifiwa miaka ya nyuma kutoka Rukururu – Mlangali ambao ulikuwa ni wa vijiji 14. Ule mradi kama ungetekelezwa, ungeenda katika vijiji vingi sana na hivyo wananchi wa kule wangeweza kupata maji kutoka katika hayo maeneo. Mpaka Vijiji vya Ibembo vingeweza kupata maji, lakini mpaka sasa hivi ule mradi haujatekelezwa na mpaka sasa hivi kuna upungufu mkubwa sana wa maji katika vijiji.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana hata takwimu mnazozisema kwamba upatikanaji wa maji vijijini umefika asilimia 80, sijui labda kwenye majimbo ya wenzangu, kwenye jimbo langu sidhani kwa sababu vijiji vingi bado havina maji safi na salama. Kwa hiyo, hizo takwimu labda pengine zina- fit zaidi kwenye maeneo mengine kuliko katika Jimbo la Vwawa.

Mheshimiwa Spika, kuna mradi wa maji ambao ulitekelezwa kutoka kwenye Kijiji cha Idiwiri kwenda Iyura na ukaenda katika vijiji saba. Sasa kitu cha ajabu ni kwamba ule mradi yale maji yanatoka kwenye Kata ya Idiwiri, kwenye Kijiji chenyewe cha Idiwiri ambapo maji yanatoka hakikupata maji; Kijiji cha Iromba ambako maji yanatoka hakijapata maji; Vijiji vya Mafumba havina maji; vijiji vingine maji yanatoka pale yanaelekea kwenye vijiji vingine.

Mheshimiwa Spika, sasa wananchi wa maeneo yale wamekuwa na malalamiko makubwa kwamba wanatakiwa kutunza vyanzo vya maji, wanatakiwa kuhakikisha maji yanakuwepo, lakini wao wenyewe hawajapatiwa maji. Namuomba Mheshimiwa Waziri, hebu lipe uzito, liangalie hilo eneo ili nao waweze kupata maji.

Mheshimiwa Spika, kuna Kata ya Nanyara; kuna Vijiji vya Songwe, Songwe - Rusungo, Namronga na maeneo mengine. Kuna mradi wa maji wa mwaka 1972 ambao kwa kweli mabomba yamechakaa sana, umekuwa haufanyi kazi. Mpaka sasa hivi kumekuwa na shida sasa ya upatikanaji wa maji na kwa sababu wakati ule wana-design ule mradi wananchi walikuwa ni wachache, sasa hivi wamekuwa wengi, bado hakuna upatikanaji wa maji wa kuweza kutosha katika lile eneo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba katika miradi ambayo wanaenda kuitekeleza kwenye vijiji, basi wakaliangalie hilo eneo ili vijiji vile viweze kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, kuna Kijiji cha Ihoa, Welutuu na Ruvumbila, naomba sana tukaviangalie.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza, naomba niipongeze sana Wizara ya Nishati kwa kazi kubwa ambayo wameifanya. Kwa kweli wamefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara hii inashughulikia masuala ya nishati ambayo ni muhimu sana katika maendeleo ya Taifa letu. Naamini kwa miradi mikubwa ya kimkakati ambayo wameianzisha, miradi kama ya SGR, Nyerere, Bomba na kadhalika, kwa kweli wakiisimamia vizuri itatoa mchango mkubwa sana katika maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nizipongeze taasisi ambazo ziko kwenye Wizara hii zinafanya kazi nzuri sana. Ni kwa mara ya kwanza nimesikia TANESCO wamepata faida kubwa, kwa kweli nawapongeza sana, nina imani kazi hii itaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunahitaji nishati na Serikali ya Awamu ya Sita imetenga fedha zaidi ya shilingi trilioni 2.3 ili mambo kadhaa yajitokeze katika nchi hii. Sasa kwa sababu ya muda nitasema mambo makubwa matatu.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, nishati itasaidia kuhakikisha kwamba kunakuwa na maisha bora kwa Watanzania wote. Watanzania wanaoishi mijini na vijijini, wanahitaji umeme wa uhakika, wanahitaji gesi, mafuta na kadhalika. Kwa hiyo, nina imani fedha hizi ambazo Serikali imewekeza zitachochea sana kuhakikisha maisha ya Watanzania yanaimarika na umaskini unapungua kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, fedha hizi zilizotengwa tunategemea zitatengeneza ajira nyingi kwa Watanzania ambalo limekuwa ni tatizo la muda mrefu. Ajira zitakazotengenezwa katika bomba la mafuta, gesi, mafuta na vituo vya mafuta, zitawasaidia Watanzania. Nina uhakika kwamba iwapo vitasimamiwa vizuri, vitasaidia sana Watanzania kule vijijini kuanzisha biashara, kufanya kila aina ya kazi kwa sababu hivi vitu ni muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, nishati ya uhakika itasaidia na kuhakikisha tunajenga viwanda vitakavyozalisha bidhaa mbalimbali za Tanzania. Hatuwezi kujenga viwanda imara kama nishati itakuwa siyo ya uhakika au kama tutakuwa na umeme unaokatikakatika. Kwa mfano, kama sasa hivi katika Mkoa wa Songwe, kuna tatizo kubwa sana la kukatika kwa umeme kila mahali. Unaweza ukakatika zaidi ya mara kumi kwa siku na kuna maeneo mengi hayana umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi nzuri ambayo wameifanya REA na ambayo Mheshimiwa Waziri ameifanya lakini vipo vijiji karibu 31 kwenye Jimbo la Vwawa havina umeme hadi sasa hivi. Bado kuna mitaa kadhaa haina umeme, Mitaa kwa mfano Isangu, ni kijiji lakini hakina umeme; Mitaa ya Rondoni na Shanko, kote hawana umeme. Vijiji kama Idunda, Ipyana, Iromba, Namwangwa, Nyimbili, Hantesya, Izumbi, Sakamwera, Mponera, Ipunga, Ipapa, Mpanda, Masangura, Ihoa, Welu II, Idibira, Rusungo, Namlonga, Maroro, Isararo, Sakamwera, Mantengu, Chizumbi, Rudewa, Msambavwanu, Kilimampimbi na Kata nzima ya Nyimbili; vyote havina umeme hadi sasa. Pamoja na kazi nzuri anayoifanya Mheshimiwa Waziri, naomba vijiji hivi vyote vipatiwe umeme kama alivyosema na naamini tutakuwa tumefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri amesema nguzo hazilipiwi na wananchi watalipa Sh.27,000 wale ambao mitaa yao inafanana na vijiji. Mimi katika Jimbo la Vwawa bado ni vijiji na ndiyo maana tumeshindwa kupata sifa ya kuwa Manispaa kwa sababu maeneo mengi bado ni vijiji lakini mpaka leo hii ukienda TANESCO wanakwambia lazima ulipie nyaya na nguzo na wanakwambia kwamba sisi hatuhusiani na REA labda ukitaka hivyo nenda REA, REA wanakwambia huko TANESCO.

Naomba masuala haya yaangalie vizuri toeni waraka wa kuwaelekeza watendaji wa TANESCO ili wazingatie maagizo ya Wizara. Ikitokea Wizara mnatoa maagizo na TANESCO wanasema sisi hatutekelezi, hatuna waraka, kwa kweli mnaleta usumbufu mkubwa sana kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipatia hii nafasi ili niweze kutoa mchango wangu katika sekta hii ya Maliasili na Utalii. Jambo la kwanza, nawapongeza sana viongozi wa Wizara kuanzia kwa Waziri, Naibu Waziri, Watendaji wote na Wahifadhi wote wamefanya kazi nzuri sana, pamoja na changamoto ambazo zinawakabili kutokana na ugonjwa huu wa COVID 19. Hongera sana kwa kazi ambayo wameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kabisa kwamba, sekta ya utalii ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu, sisi sote tunajua hilo, mchango wake kwenye pato la Taifa, kwenye ajira na kwenye fedha za kigeni ni kitu muhimu sana. Hata hivyo, wengi wanasema Tanzania ni nchi ya pili duniani kwa kuwa na vivutio vingi vya utalii, lakini nafikiri kwa sasa hivi ni nchi ya nane, sio ya pili tumeshaharibu, tumeshavuruga vuruga kwa hiyo, sasa hivi Tanzania sio ya pili tena bali ni nchi ya nane.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ili nchi iweze kunufaika na vivutio vya utalii vilivyopo, lazima tuchukue mikakati ya makusudi ya kuhakikisha kwamba, tunaiendeleza hii sekta ya utalii. Sasa ili kufanya hayo nitapendekeza mambo machache, lakini kwa sababu ya muda sitaweza kuyasema yote. Nataka kusema kwamba, nchi yetu ina bahati ni nchi yenye Mlima mrefu kuliko milima yote katika Afrika. Ni nchi ambayo mwanadamu wa kwanza wa kale alipatikana Tanzania. Ni nchi yenye Maziwa, ni nchi yenye bahari, yenye milima, yenye kila kitu, lakini tatizo tulilonalo hatujaweka mikakati ya kutosha ya namna ya kutumia huu utajiri ambao Mungu ametupatia. Kwa hiyo, tufike mahali tuweke mikakati ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia sasa hivi nchi kumi zinazoongoza kwa utalii duniani Tanzania hatumo. Inaanza Ufaransa ambayo ina watalii milioni 89, kuna Spain milioni 82, USA milioni 79, China milioni 62, Italy milioni 61, Turkey milioni 45, Mexico milioni 41, German milioni 38, Thailand milioni 38, UK milioni 36, Tanzania hatumo wala Afrika hatumo, pamoja na utajiri wote huu tulionao. Hivyo, ni lazima tukae chini tujiulize kwa nini sisi tunakosa kuweka mikakati ya makusudi na kuweka uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ambalo lazima tuhakikishe tunalifanya, ni kutengeneza miundombinu thabiti ya kuvutia utalii nchini. Hii Serikali wameanza kufanya vizuri, lakini hapo katikati tumeshajichanganya. Tumeamua kuchukua mapato ya utalii yale tumeyapeleka kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Sasa tunaziacha Taasisi za Uhifadhi hazina fedha za kujenga miundombinu, halafu tunataka kujenga utalii, nani atatangaza utalii? Tutauendelezaje katika utaratibu wa namna hii? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani kuna haja ya kukaa chini na kulitafakari, ili tuone haya Mashirika ya Hifadhi sasa yawe na mapato yake, yawekeze, yajenge miundombinu, watu waende mahali sehemu mbalimbali, wakale maisha, hapo ndio tutaijenga nchi yetu, bila kufanya hivyo hatuwezi kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Mbozi kuna Kimondo cha aina yake, ni moja ya vimondo nane duniani, kiko pale Mbozi. Naishukuru Serikali imewekeza pale, lakini bado hatujakitangaza vya kutosha. Tunayo maji moto kule Mbozi, hatujatangaza vya kutosha. Sasa na maeneo mengine yote ya mali kale ambayo hatujayatangaza lazima tuwe na mkakati wa namna ya kutangaza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nini tunatakiwa kufanya katika kutangaza? Tunayo TBC, Channel Two ambayo tuliweka mahususi kwa ajili ya kutangaza, lakini je. hiyo ndiyo itawafikia watalii wote tunaowahitaji? Lazima tutafute namna ya kutangaza utalii, tutumie mbinu gani, tuwekeze, bila kuwekeza hatuwezi kupata vitu. Hatuwezi kupata fedha, lazima tuwekeze kwenye matangazo ya kutosha ili kuweza kuvutia utalii. Hapa Dodoma kwa mfano, Bunge tumekaa miezi minne niambieni ni sehemu gani ambapo sisi tumeenda kula maisha, wapi? Sijapaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujawekeza vya kutosha, kwa hiyo, lazima tuweke mkakati kuwekeza ili kusudi watu wahakikishe kwamba wanaenda kula maisha. Naomba kwa sababu, Kamati imependekeza, tuanzishe Mamlaka ya Kuendeleza Utalii. Naunga mkono hii mamlaka ni muhimu sana, ikafanye hii kazi, ikalitangaze Taifa letu, ikatangaze vivutio vyetu, tuweze kuleta maendeleo, tuweze kupata fedha nyingi, tuweze kutengeneza ajira mbalimbali kwa Watanzania, hii itakuwa ni kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati imependekeza tuanzishe Mamlaka ya Misitu Tanzania badala ya kuwa Wakala. Naunga mkono, lakini nitaunga mkono tu wakimaliza tatizo lililopo Mkoa wa Songwe la matumizi ya mkaa. Walizuia wananchi kwamba, wasitumie mkaa, wasivune mkaa, lakini tunajua kabisa matumizi ya mkaa yapo, lazima yawekewe utaratibu mzuri na wananchi wa Songwe wapate sehemu hiyo, hiyo itawasaidia sana. Kwa hiyo, nitaunga mkono kama haya mambo yatakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusema bahati mbaya naona muda haukuwa upande wangu, lakini niwahamasishe Watanzania twende tukale maisha, ndipo tutajenga uchumi imara. Tafuta fedha, katumie, utapata maendeleo, Mungu awabariki, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nianze kwa kuunga mkono hoja ya Uanzishwaji wa Eneo Huru la Biashara la Nchi za Afrika. Kwa kweli nafikiri hili Azimio limekuja kwa wakati wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kulileta Azimio hili ambalo ni muhimu sana, lakini pia naipongeza sana Kamati ya Viwanda na Biashara kwa kuchambua kwa undani sana Azimio hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ina historia ndefu. Nchi yetu imekuwa ni nchi ambayo iliongoza mapambano ya ukombozi wa Afrika wa kisiasa na nchi zetu zote zimepata sasa uhuru, lakini tunabaki nyuma katika kuongoza mapambano ya ukombozi wa kiuchumi, Sasa hili Azimio lengo ni kuleta ukombozi wa kiuchumi. Ndiyo maana lengo la Azimio hili ni kuchochea uchumi na biashara katika nchi za Afrika. Kwa hiyo, mimi nafikiri ni wazo ambalo ni zuri sana.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu tusibaki nyuma, kila wakati tunatakiwa tuwe mbele, kama tulivyoongoza mapambano ya kupata uhuru tuongoze na mapambano ya kuleta uhuru wa kiuchumi. Kwa hiyo, hili mimi nafikiri lazima tuwe mbele. Pili, nchi yetu imekaa kijiografia mahali pazuri (strategically located). Sasa lazima tutumie fursa hii ya nchi yetu kuwa strategically located ili tuweze kunufaika na biashara ya nchi hizi ambazo tumezisaidia sana katika kuleta ukombozi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukua hali ya biashara Bara la Afrika linatisha. Sisi tunafanya biashara katika nchi za Afrika kwa asilimia 17, nchi za Ulaya asilimia 69, nchi za Asia asilimia 60, Mabara mengine yote ni zaidi ya asilimia 60. Kwa hiyo, umefika wakati lazima tufanye biashara na sisi, tufufue tuweze kufanya vizuri. Na mimi ninaamini hili litatusaidia sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninao mfano hai. Nimeona kwa mfano wananchi wa kule Songwe wanavyopata shida hasa inapokuja katika kufanya biashara na nchi za jirani. Tuko pale karibu tunapakana na Malawi na Zambia, tuko ni lango la SADC lakini tunapata shida kwa sababu ya kutokuwa na misingi na mambo mazuri ya kufanya biashara katika hizi nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano pale Tunduma unakuta kwamba wananchi wanaagiza mbolea Zambia, ina bei ya chini sana, iko bei ya chini kabisa, lakini ukichukua mbegu ziko bei ya chini sana na ziko mbegu nzuri kabisa zinazofaa kwenye kilimo. Wananchi wale wakienda kununua kule wanapoziingiza Tanzania wanavyofukuzwa, wanavyokamatwa utafikiri wamefanya uhaini. Kwa hiyo, hili suala mimi nafikiri kwamba tukianzisha haya maeneo yanatusaidia sana katika kuweza kutuachia biashara katika maeneo ya namna hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo ambayo lazima tuyazingatie na Mheshimiwa Waziri na Serikali lazima tufanye kazi kubwa ya kuhakikisha kwamba tunahamasisha ili nchi yetu iweze kupata manufaa ya hili Azimio.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ni tija. Tija katika bidhaa zetu kwenye kilimo iko chini, kama wenzangu walivyosema. Tija kwenye bidhaa zetu iko chini, bidhaa zetu haziwezi kushindana na bidhaa kutoka maeneo mengine. Kwa hiyo ni wajibu wetu sisi kuhakikisha kwamba tunaongeza tija ili bei iwe nzuri ili zi-meet ubora unaotakiwa wa kuweza kushindana katika hii biashara. Mimi naamini hiyo itatusaidia sana tukiweza kuifanya hivyo. Wameweka mifano ya bidhaa za kilimo, wameweka bidhaa mbalimbali mimi sitaki kurudia, lakini nataka kusema kwamba hilo ni suala la msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, tunapoenda kufanya biashara swali ambalo ni lazima tujiulize ni biashara ya namna gani tunakwenda kufanya. Tunasema kama ni biashara ya kuuza malighafi hiyo ni biashara mbaya. Biashara inatakiwa ukauze bidhaa zilizoongezwa thamani, hiyo ndiyo biashara ambayo inatakiwa tuingine nayo katika Bara la Afrika. Hapa tusijipe moyo kwamba tunakwenda kuuza malighafi au tunakwenda kufanya nini, hiyo haitatusaidia kwa sababu tunayo matatizo ya msingi katika nchi hii ambayo ni kupunguza umaskini na kutengeneza ajira kwa watu wetu. Ili tuweze kufikia hayo yote lazima tujenge viwanda imara, tuongeze thamani ya bidhaa zetu, ndiyo tutaweza kutoa ajira na ndiyo tutaweza kupunguza umaskini wa watu wetu katika maeneo mbalimbali. Kwa hiyo, mimi nafikiri mkazo lazima uwe katika kuongeza thamani ya mazao yetu, ndiyo tutaweza kushindana vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo eneo lingine katika nchi za Afrika ambalo lazima tubadilike kifikra. Tuanze kujenga uaminifu, Waafrika walio wengi si waaminifu. Katika biashara sasa hivi tunazoenda kushindana tunaenda kushindana na baadhi ya nchi wapo watu ambao si waaminifu. Kwa hiyo na sisi lazima tujitahadhari na watu wetu wawe waaminifu. Ujue kabisa kwamba ukikopa unatakiwa ulipe, ukifanya biashara, ukiingia mkataba u-deliver. Kama inatakiwa upeleke bidhaa ndani ya wiki moja upeleke ndani ya wiki moja. Tukiendelea na uswahili wetu ambao tumeuzoea huu mimi nadhani kwamba hatutaweza kufanikiwa na kuona manufaa mapana ya azimio hili ambalo nafikiri ni muhimu sana katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nataka kusema kwamba hili Azimio limekuja kwa wakati muafaka tuliunge mkono, tushikamane na Serikali tuhakikishe kwamba kweli tunaenda kunufaika na Azimio hili na wananchi wetu waandaliwe vizuri, wapewe elimu ya kutosha ili waende sasa, twende tukafanye biashara katika hizi nchi za Afrika na sisi tufungue mipaka na masoko ya bidhaa zetu yapatikane.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote niungane na Wabunge wenzangu kukupongeza wewe pamoja Naibu Spika kwa kuchaguliwa kwa asilimia 100, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati hizi mbili ambao kwa kweli, wamefanya kazi nzuri sana katika kuwasilisha taarifa, lakini pia kamati zimechambua kwa kina sana mambo mbalimbali ambayo yanaonekana na haya ndio machache ambayo yameweza kuja ambayo mimi naamini kwamba, yana vitu vya msingi ambavyo Serikali inatakiwa iende ikavifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wote tuunge mkono maazimio yaliyoko katika taarifa hizi, ili Serikali iende ikayafanyie kazi. Na ikiyafanyia kazi ituletee mrejesho namna ilivyotekeleza haya maazimio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama taarifa zilivyobainisha, yapo maeneo ambayo yamekuwa yana matumizi yasiyoridhisha. Maeneo ni mengi, lakini katika Serikali ukichukua Wizara, ukachukua mashirika, ukachukua idara zinazojitegemea, ukachukua wakala, maeneo mbalimbali yanaonekana kuwa na viashiria vya matumizi yasiyoridhisha. Na maeneo hayo ni pamoja na maeneo ya utengenezaji wa mifumo.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi mifumo mingi imekuwa ni kichaka ambacho kinatumika katika matumizi mabaya ya hela za umma. Kwa hiyo, nitaliomba Bunge lije liangalie katika taasisi zote mifumo yote ambayo tumeitengeneza kwa muda wa miaka mitano au kumi mpaka tulipofika tumetumia fedha kiasi gani? Na hiyo mifumo imeleta nini kwenye Taifa hili? Hilo ni eneo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo limekuwa ni shida ni kwenye eneo la manunuzi na usimamizi wa mikataba. Kwa sababu ya muda, sitaweza kuyazungumza kwa undani. Lakini katika hili eneo ndio maana tumeona kwa mfano bandari peke yake, hiyo tumeweka ni mfano tu, bandari peke yake mifumo bilioni 17 na kitu zimetumika, lakini mifumo ile haina tija. Sasa hivi wameondokana na mifumo hiyo, mifumo haionani, sasa wanakuja na mfumo mwingine, tena zinahitajika hela nyingine, sasa hii kwa kweli haikubaliki. Na taasisi nyingine nyingi ambazo mimi kwa sababu ya muda sitaweza kuzisema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hebu tuje kwenye hali halisi, TRA wanaonekana kwenye makusanyo wana trilioni 360 ambazo ziko kwenye Bodi ya Rufaa ya Kodi. Hivi ni sura gani inayoonekana kwenye Serikali?

Mheshimiwa Spika, yani tunaposema Serikali inadai hizo hela, nimeliangalia hili deni mwaka 2015 mpaka 2016 deni lilikuwa ni 1.3 trillion. Mwaka 2017 deni lika-shoot mpaka trilioni 360; nazungumzia trilioni ambazo ukizigawa ni bajeti ya nchi hii ya miaka 10 hizo hela kama zingekusanywa, lakini hebu tujiulize hivi hili deni lina uhalisia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeangalia kwenye vitabu vyote vya TRA, vitabu vya Serikali, vitabu vya kiuhasibu, hili deni halipo. Na hili deni linatokana kwa kiwango kikubwa na makinikia, lile deni la makinikia. Sasa kama tumefanya majadiliano na zile kampuni zinazohusika tumemaliza, hili deni nashauri Serikali iangalie uwezekano ilifute linachafua taswira nzuri ya Serikali. Kwa hiyo, nafikiri hili lazima waliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili; yapo mashirika mengi ambayo yanaonekana yana upungufu mkubwa, yana shida ya fedha. Nianze kwa mfano Shirika la Ndege linaonekana lina upungufu mkubwa, lina madeni bilioni 246 ambazo tunafikiri Serikali iangalie uwezekano wa kuiongezea ili mizania ya hesabu ikae vizuri, lakini kuna TANESCO. TANESCO kuna bilioni 493.6, lakini TANESCO hiyo inadai kwa wateja bilioni 422, sasa mizania yake haijakaa vizuri. Ukienda TPDC wanaidai TANESCO fedha nyingi sana, lakini kwenye TPDC pia kuna deni la ujenzi wa bomba la mafuta ambalo Serikali inalipa tayari, lakini kwenye vitabu halifutiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nafikiri Serikali, haya yanachafua. Ni vizuri mkaangalia namna ya kusafisha vitabu vikae vizuri, mizania zile zikae vizuri, kuliko hali iliyoko sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waliunganisha kweli benki wakaamua kuunganisha, hivi Serikali unapochukua benki inayofanya vizuri unaunganisha na benki isiyofanya vizuri, lengo linakuwa ni nini? Halafu unawachukua wale wafanyakazi walioshindwa kuiendeleza benki, walioharibu, unawaleta kwenye benki inayofanya vizuri. Hii haijakaa vizuri kabisa. Halafu unachukua madeni chechefu yaliyoshindikana kulipwa huko, unayaleta kwenye benki inayofanya vizuri, maana yake sasa mizania ya benki inayofanya vizuri sasa inaharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafikiri hili siyo lengo, lengo la Serikali inawezekana lilikuwa zuri, zile benki zenye madeni chechefu waziundie kampuni yao huko zinazofanya vizuri waziache zifanye vizuri. Hiyo itasaidia sana na naona kuna hizo sitaki kuzitaja kwa sababu ya muda, naona mambo karibu yamekwisha, lakini nataka niseme moja kwa dakika moja.

Mheshimiwa Spika, kuna benki zinazodaiwa, kuna Serikali inadaiwa trilioni 1.1 na NSSF, lakini Rais wetu amefanya kazi nzuri. Toka miaka nenda rudi tunadai ule Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa Serikali zaidi ya trilioni mbili na kitu, ametoa non cash bond kwenye hiyo, amenusuru.

Mheshimiwa Spika, sasa tunamwomba na NSSF aangalie na haya mashirika mengine nayo aangalie, lakini hii tume ya madini ya bilioni 156 wafanye …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa sasa hapo tena muda umetuacha kidogo.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, naomba wafanye reconciliation.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja zote na Mungu awabariki. Ahsante sana. (Makofi)
Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi. Niunge mkono hoja ya Mheshimiwa Ezra, kwa namna alivyoiwasilisha hapa Bungeni na kwa namna hili tatizo linavyotukabili sisi wote katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, katika eneo langu kwenye Jimbo la Vwawa, nimepigiwa simu na watu wa zaidi ya 36 wakilalamika kwamba wamekosa mikopo na wengine waliahirisha mwaka jana wakawa na matumaini kwamba mwaka huu watapata, lakini hawajapata na hali ilivyo tatizo ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema ni kwamba hili tunalolijadili pengine tunaweza tusipate ufumbuzi kwa leo na tunaweza tusilijadili kadri inavyowezekana, lakini naliona kwamba lazima tuje na majawabu ya muda mfupi na tuje na ya muda mrefu. Sasa kwa muda mfupi nitapendekeza nini kwamba ambacho tunafikiria kwa sasa hivi. Kwa sababu nchi yeyote bila kuwa na maarifa, bila watu wake kuwa na maarifa ya kutosha. Watu bila kuwa na ujuzi huwezi kujenga uchumi imara na huwezi kuleta maendeleo ndani ya nchi ile.

Mheshimiwa Spika, ndio maana Serikali ya Awamu ya Sita, imeamua kuweka uwekezaji mkubwa kwenye hili eneo. Ukiangalia namna tulivyowekeza kwenye shule za msingi, shule za sekondari, ukiangalia madarasa yanayoendelea kujengwa, vyuo vinavyoendelea kupanuliwa, kwa uwekezaji huu ni kwamba tunataka tuijenge jamii iliyoelimika, yenye ujuzi ambao ni mahiri, itakayoweza kuleta maendeleo ya nchi yetu na ndio tutaweza kupambana na umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa katika uwekezaji huu wa shule za msingi na sekondari ni lazima uwiane na namna tunavyowapeleka kwenye vyuo vya elimu ya juu na vyuo vya kati. Sasa hivi hapa pana changamoto, nafikiri lazima Serikali ituambie tunafanyaje ili tuweze kujinasua hapa. Bodi hii ya Mikopo imekuwepo kwa zaidi ya miaka 17. Ni wazi na mafanikio yapo, lakini zipo changamoto ambazo lazima tuziangalie kwa undani. Tuangalie suala la kibajeti, bajeti iliyo ukiangalia na idadi ya udahili inatosheleza? Lipo suala la muundo wa Bodi namna inavyotekeleza majukumu yake, kama taasisi, je, katika hali tuliyonayo, mazingira ya leo, huu muundo wa bodi unatosheleza? Katika hali tuliyonayo vigezo vinavyotumika katika kuwapatia watoto mikopo au kutowapatia, hivyo vigezo vinatosheleza? Namna tulivyojipanga kugharamia hii mikopo tumejipangaje? Kwa hiyo nafikiri yapo mengi ambayo ni ya msingi ili tuweze kujinasua.

Mheshimiwa Spika, sasa nataka kupendekeza kwamba katika hali ya udharura iliyopo Serikali ituambie ina Bajeti ya shillingi ngapi ambazo imepata sasa hivi? Pia Bunge hili kwa sababu ndilo linalopitisha Bajeti, tuangalie kama inawezekana zikatafutwa fedha mahali pengine popote kama tulivyofanya wakati tulipokuwa na crisis ya kwenye kilimo, kama tulivyofanya katika maeneo mengine ili tuwekeze kwenye hili eneo angalau tuvuke kwa kipindi hiki, hii itatusaidia sana.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa suala la muda mrefu, Wizara ifanye mapitio ya kitaasisi, ya kimuundo na kuangalia je, muundo tulionao huu unakidhi mahitaji ya leo ya sayansi na teknolojia? Naamini kwa kufanya hivyo, najua jitihada zimechukuliwa na Serikali, nimemsikia Waziri ameunda tume, amefanya nini, lakini ya msingi ya dharrla lazima kwanza tuje na Bajeti ya kutatua hili tatizo ndiyo tujipange sasa kwa siku zinazokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile la pili, tufanye mapitio ya sheria iliyopo, je, hii sheria inatosheleza? La tatu, tufanye mabadiliko ya mfumo wa utoaji wa mikopo na la nne tuangalie sasa mipango ya kupata fedha, siyo tu kwa upande wa Serikali bali tushirikishe na wadau wengine kuweza kuongeza fedha katika hili eneo na ikiwezekana badala ya kuitwa Bodi ya Mikopo iwe ni Mfuko wa Elimu na ikiwa Mfuko wa Elimu, isiwe elimu ya juu tu hata elimu ya kati.

Mheshimiwa Spika, najua kuna tatizo la muda, basi nasema naunga mkono hoja na naamini Serikali itakuja na tamko kwa suala hili la dharura. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu katika mwelekeo wa mpango wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. Pia naipongeza Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuja na mwongozo huu wa Mpango na Bajeti ambao wameileta mbele yetu. Tatu, naipongeza Kamati ya Bajeti kwa namna walivyoichambua na kuleta maoni yao hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wetu lazima ujielekeze katika kujibu mambo ya msingi yanayotuhusu. Ninafurahi kuona kwamba mpango huu umeandaliwa vizuri. Mwelekeo wa mpango huu ni mzuri na unatupeleka kule tunakotaka. Yapo matatizo ya msingi ambayo sisi sote tunahusika na lazima tutafute mwelekeo wa namna ya kuyatatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ni umasikini mkubwa wa wananchi katika utajiri ulio mwingi katika nchi yetu. Nchi yetu ni moja ya nchi tajiri sana, lakini watu wake ni masikini. Kwa hiyo, hili ni lazima mwelekeo wa mpango ukajibu hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni ukosefu na upungufu wa ajira kwa vijana wetu; na la tatu, ni mchango mdogo wa sekta za uzalishaji kwenye pato la Taifa. Jambo la nne, ni tija ndogo katika maeneo mbalimbali; na la tano ni ukuaji mdogo wa sekta ya viwanda na mambo mengine yote. Haya mambo matano ni msingi mkubwa wa utayarishaji wa mpango. Nami naamini kwamba mpango huu unatupeleka katika kujibu na kutafuta ufumbuzi wa haya ambayo yanaikabili nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, ukisoma Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2000-2025, ina vipaumbele vitano. Moja ya kipaumbele ni kwamba tunataka kuboresha hali ya maisha ya Watanzania. Sasa hivi maisha ya Watanzania katika uhalisia, hali ni mbaya. Tunataka kuwepo kwa mazingira ya amani, usalama na umoja, na hili tumefanikiwa kwa kiwango kikubwa; tunataka kujenga utawala bora; tunataka kuwepo kwa jamii iliyoelimika na inayofundishika; na tunataka kujenga uchumi imara unaoweza kukabiliana na ushindani wa nchi jirani na nyinginezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia dira yetu inavyosema, mipango yetu, vipaumbele vyetu, Sera na Ilani ya Chama cha Mapinduzi, vyote vinashabihiana. Vinatulazimisha tukae chini tuweze kutatua haya matatizo ya wananchi. Sasa hali ilivyo sasa hivi, tunazo takwimu nyingi; tunayo nchi yetu ambayo imebarikiwa kuwa na rasilimali za kila namna, lakini tunazunguka katika mzunguko wa umasikini (poverty cycle), tunazunguka mle. Sasa hapa lazima tujikite kuona tunatokaje katika huu mzunguko ili twende kwenye eneo lingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mipango yetu na mambo yote ambayo tumekuwa tukiyafanya, bado tunazunguka. Sasa hivi kuna mjadala mkubwa kwamba nchi yetu ilikuwa imefika kipato cha kati, sasa tumerudi kipato cha chini, lakini sisi kazi yetu ni kuhakikisha kwamba tunatoka hapo tunaenda mpaka kwenye kipato cha juu. Sasa yapo mambo ambayo mimi ningependekeza kwamba tuyaangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumependekeza kwa muda mrefu na bado halijafanyiwa kazi. Kwanza, ni uwepo wa Tume ya Mipango pamoja na Baraza la Tija.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongezae Mheshimiwa Mbunge kwa mchango mzuri. Nimeona ame-refer hili jambo lililosemwa juzi kwamba Tanzania tumeshuka kwenda kwenye kipato cha chini, pamoja na kwamba nimejiandaa kuja kulijibu, lakini niliona ili kumsaidia atiririke vizuri, ni kwamba Tanzania haijashuka kwenda kwenye kipato cha chini na taarifa zilizotolewa na mchangiaji, Mbunge wa Musoma Vijijini siyo sahihi, na nukuu aliyonukuu na yenyewe haikuwa sahihi. Nadhani nitatolea zaidi ufafanuzi nitakapokuwa na-wind-up.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hasunga, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea, kwa sababu sina tatizo kabisa katika huo mjadala unaoendelea. Naipokea kabisa kwa sababu tunatakiwa tuwe na takwimu sahihi, na ndiyo msingi wa kupendekeza kwamba tuwe na Tume ya Mipango itakayokuwa na uwezo wa kuchambua hali ya maisha, uchumi wa nchi yetu na kutupa takwimu sahihi. Ile Tume ya Mipango itapanua wigo, itafanya watu wote waweze kushirikishwa wataalam mbalimbali, waweze pia kujadili watupe takwimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiri Mheshimiwa Waziri hii itatusaidia sana kuwepo kwa Tume ya Mipango lakini pia na Baraza la Tija ambalo litasimamia kupanua tija katika uzalishaji, tija katika viwanda vyetu na tija katika maeneo mbalimbali. Hili ni suala ambalo nafikiri ni la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tumeona nchi yetu iko strategically located, na ndiyo maana sasa hivi tunazo bandari ambayo tunafikiri zinaweza kuhudumia nchi jirani. Sasa hivi kuna mjadala unaoendelea, watu wengine wanasema tujenge Bandari ya Bagamoyo na wengine wanakataa. Mimi nafikiri Bandari ya Bagamoyo ni inevitable, lazima tuijenge, na Bandari ya Dar es Salaam iendelee, ya Mtwara iendelee na bandari nyingine zitakazowezekana zijengwe. Kwa sababu lengo la hizi bandari ni kuhudumia, na tunataka zile nchi ambazo hazina uwezo wa ku-access ziweze kuhudumiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye hili lazima tuweke nguvu. Kwa hiyo, nategemea mpango huu utakapokuja, utakuja na namna ya kuijenga hii Bandari ya Bagamoyo, lakini tusisahau na pale Bandari Kavu Mpemba, Tunduma kwa sababu pale ndiyo lango la SADC. Pale ndiyo nchi za Zambia, Malawi na nchi zote zitakuja kuchukulia mizigo pale. Kwa hiyo, tukijenga Bandari ya Bagamoyo, tunajenga Bandari Kavu pale Tunduma-Mpemba, tutakuwa tayari tumeitendea haki nchi hii. Tutaenda kujibu matatizo haya ya msingi ambayo nimesema yapo katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ambalo napenda kupendekeza, ni katika upande wa allocation ya resources. Mheshimiwa Waziri atakapokuja na bajeti, nimeona mwongozo, nimeusoma, lakini nadhani, ili tuondoke katika mzunguko wa umasikini ili tutoke pale, uwekezaji tuje na formula ya namna ya kuwekeza zile rasilimali zetu. Allocation ya resources zile za maendeleo, tuje na formula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza napendekeza, zaidi ya asilimia 30 au 40 ielekezwe kwenye sekta za uzalishaji. Kwa sababu tukielekeza kwenye uzalishaji, huko ndiyo wananchi wengi wapo; tutatatua tatizo la ajira, umasikini na tutahakikisha uzalishaji malighafi zinapatikana na ndiyo viwanda sasa vitaweza kujengwa, tutapata malighafi. Huwezi kufanya hivyo kama hilo halitakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 30 iende kwenye huduma za jamii na asilimia 30 nyingine iende kwenye huduma za biashara na miundombinu. Hiyo formula inaweza ikatusaidia kutoka. Tukiwekeza kwenye huduma za jamii bila kuwekeza kwenye uzalishaji, tutakuwa tunazunguka kwenye poverty line, hatutatoka kule kwenye yale maeneo ambayo mimi ningependekeza tutoke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la nne, kujenga viwanda na kuanzisha mfuko wa kuchochea viwanda. Hatuwezi kujenga viwanda kwa kupiga kelele. Hatuwezi kujenga viwanda kwa kusema tunahamasisha viwanda, lazima tutenge fedha, tujenge viwanda, halafu tutafute waendeshaji wa hivyo viwanda. Yale mazingira yawe yameshatengenezwa, tutakuwa tayari tumetekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mengi, lakini mengine tutayachangia, nashukuru sana kwa kupata hii nafasi na ninaunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza nianze kwanza kuipongeza Wizara, nampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na timu kwa ujumla kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakifanya, pia niipongeze Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwa taarifa yao nzuri ambayo wamefanya uchambuzi wa kina nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru katika taarifa zote zinaonyesha kwamba mchango wa ukuaji wa sekta ya viwanda Tanzania umefika asilimia 8.9 sasa katika mazingira tuliyonayo asilimia 8.9 ni ukuaji bado huko chini hauendani na hali halisi ya changamoto tulizonazo na mahitaji tuliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma nchi yetu ilibahatika, tuliweza kujenga viwanda vya aina zote, toka tumepata uhuru tulijenga karibu viwanda vya aina zote. Tulikuwa na viwanda kwanza ni sera ya Chama cha Mapinduzi sasa hivi, Chama cha Mapinduzi kimetoa sera ni moja ya malengo kwamba lazima tujenge viwanda na viwanda ukiviangalia ndio vitatoa suluhu ya matatizo yote tuliyonayo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huko nyuma tulikuwa na viwanda vya kuongeza thamani ya mazao. Baba wa Taifa alijenga viwanda karibu vyote vilikuwepo! Tulikuwa na viwanda vya kuchakata nyama, viwanda vya kuongeza thamani ya nyama, viwanda vya ngozi vilikuwepo na mazao mbalimbali ya Ngozi, viwanda vya misitu na mbao vilikuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na mashine viwanda vya tools za uzalishaji vilikuwepo vililjengwa, mpaka tulipofika mwaka 1974, 1975 karibu viwanda vyote vilikuwepo, viwanda vya nguo vilikuwepo, viwanda vya korosho vilikuwepo, viwanda vya mafuta vilikuwepo, viwanda vya kila kitu vilikuwepo vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabati yalikuwepo, misumari yaani hatukukosa kiwanda cha aina yoyote. Swali ambalo tunatakiwa tujiulize ni nini kilitokea viwanda hivyo vyote vikafa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukijua pale tulifeli nini ndipo tutakuwa na mkakati ambao unafaa katika kujenga viwanda kwa sasa, bila kuelewa tulikotoka hatuwezi kujenga viwanda! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara, nimesoma taarifa nafurahi wana mikakati mizuri lakini nataka hasa wanisaidie ni upi mkakati wa Wizara wa kuongeza viwanda na ajira hapa nchini ambao kweli huo mkakati tukiuangalia kama Bunge tutaridhika kwamba nchi hii itatoka hapa tulipo tutafika mahali ambapo tunataka kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la Pili ni upi mkakati wa Wizara wa kuongeza tija na thamani ya bidhaa zetu! Bidhaa zetu ni duni haziwezi kuimiri ushindani katika soko la dunia. Sasa mkakati wetu tunaouweka ni upi ili tupate bidhaa zitakazoweza kushindana katika soko la dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la Tatu ni upi mkakati wa Wizara wa kuongeza biashara ili tupate fedha nyingi za kigeni kwa sababu biashara ndio zinazoleta fedha nyingi za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la Nne, ni upi mkakati wa Wizara wa kuja na Mfuko wa Kujenga Viwanda? Hapa tutaimba! Tutaimba! hivi mfuko wa kujenga viwanda hivyo huko wapi? Je tutajenga viwanda hivyo kwa kuzungumza kwa kuhamasisha tu, au lazima tutengeneze mazingira ambapo watu wanaweza wakapata mtaji, wanaweza wakapata fedha na tunaweza tukajenga viwanda eneo tukatengeneza kabisa tukajenga baadhi ya viwanda, tukawavutia wawekezaji, wao waje na mitaji, waje na mashine lakini tuwe tumeshajenga miundombinu yote pale! Upi hasa mkakati ambao tumeuweka, hapo unafikiri ni muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni upi mkakati ambao tumejipanga kama wizara kuhakikisha kwamba tunatumia fursa zilizopo. sasa hivi, DRC wanajiunga Afrika Mashariki. DRC ni soko kubwa, tumejipangaje sasa kuhakikisha hii DRC inapokuja tunaenda kufanya biashara tunatumia fursa tuliyonayo tuweze kuchukua lile soko la DRC. Hili ni suala nafikiri ni la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ni upi mkakati wa Wizara wa kuongeza ubunifu. Tunayo SIDO, naelewa nimesoma yote lakini inatosheleza kuja na ubunifu tukawa wabunifu wa kutosha? Kwa hiyo nilikuwa nadhani tufike mahali sasa kama nchi tuangalie sekta ya viwanda na biashara ndiyo sekta mama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiuchumi tunasema uzalishaji una maeneo matatu, kuna viwanda, biashara, huduma, hizo zote ni biashara. Sasa basi kwenye viwanda tuna viwanda mama, lakini tuna viwanda kwanza vile vya kuchakata vya kutafuta malighafi yaani tunaita extractives industries ambayo tuna kilimo, mifugo, uvuvi, madini na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo vyote ni kwa ajili ya kutafuta malighafi, halafu tunakuja na viwanda sasa vya kuongeza thamani hizo malighafi ambayo tunayo, sasa hivi unajenga kiwanda cha nguo Tanzania unataka upate pamba, pamba haijazalisha kwa hiyo ina maana kama hatuta-link viwanda na biashara na kilimo hatutaweza kufanikiwa, hatuwezi kufika. Kama hatuta-link viwanda na biashara na madini hatuwezi kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hatuta-link viwanda na ufugaji na uvuvi hatutaweza kufanikiwa, kwa hiyo utakuta kwamba Wizara ya Viwanda ni mama lakini lazima ishirikiane na hizi Wizara, mkakati uwe mmoja, hapo tutaweza kufikia ile ajenda tunayoitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unakwenda pale kwenye biashara, biashara inaweza ikawa ndani inaweza ikawa biashara ya nje, inaweza ikawa ni wholesale inaweza ikawa retail, zile biashara zote ni sehemu za ajira tukipanua biashara vijana wetu wote watafanya kazi, watakuwa na ajira hatutakuwa na tatizo la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni huduma, kuna huduma za elimu, kuna huduma za afya.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hasunga, malizia sentensi yako.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ninachotaka kusema ni kwamba kwenye huduma huku ndiyo tunatakiwa tutumia hiyo nafasi. Kwa mfano, sasa hivi tumejenga vyuo vya elimu vingi sana hapa nchini viko zaidi ya 30, vile vyuo tunatakiwa tuweke mazingira vidahili wanafunzi kutoka nchi za nje ili watuletee fedha za kigeni na nchi itapata hela nyingi sana. Ninaamini kwa kufanya hivyo tutaweza kupata mchango mkubwa na uchumi wetu utakua kwa kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba kuunga mkono hoja, nawapongeza lakini nataka waje na mikakati madhubuti ambayo Bunge hili litaamini na litaweza kuyapitisha kwamba sasa tunaenda kujenga uchumi wa viwanda, tunaenda kufanya biashara, tunaenda kuongeza uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naninaunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru sana kwa kuniona na kunipa nafasi hii adimu na mimi niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwapongeze sana Wizara kuanzia Waziri na timu kwa ujumla na kwa kweli kuja na hotuba ambayo inaonesha mabadiliko mengi ambayo yanakwenda kufanyika na yale mambo saba ambayo umeyasema kwamba mnakwenda kuyatekeleza basi sisi tupo tayari tunayasubiri utekelezaji na tunaamini yataweza kuisaidia nchi hii ikaweza kwenda mbali. Kwa hiyo, Mheshimiwa Profesa tupo pamoja na wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza Kamati kwa uchambuzi walioufanya wamefanya vizuri, kwa kweli wamezungumza mambo ya msingi na mimi naamini Wizara itakuwa imeyachukua kwenda kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi ya Japan ni moja ya nchi zilizoendelea sana, lakini ilifika mahali kuna kipindi nchi ile uchumi wake ulisimama, kila kitu kilisimama. Sasa Waziri wa Elimu wa nchi ile alichokifanya alitayarisha questionnaire akawaandikia Maprofesa 14 duniani wa vyuo vikubwa, akawaambia nataka mniambie hivi hasa nini roho ya elimu katika: akaweka kila eneo kama ni kwenye kilimo, ufugaji, uvuvi, viashara, viwanda na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, wale Maprofesa walipomjibu ndiyo waliyoisaidia kuikwamua Japan na uchumi wake ukaanza tena kupiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo na sisi hapa leo Profesa umebeba hiyo dhamana, tunaelewa kwamba elimu ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu, elimu ndiyo inatupatia maarifa ya namna ya kufanya mambo yetu. Elimu inatupatia ujuzi lakini elimu inasaidia kubadilisha tabia tulizokuwa nazo halafu ziwe katika hali tunayoitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wale Maprofesa walisema, elimu hata ukisoma iwe ni Tanzania, iwe ni nje ya nchi yale maarifa unayoyapata, ukija nayo nyumbani kwako yakusaidie kuboresha mazingira uliyonayo na vitu ulivyonavyo ili viweze kuwa katika hali nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kule Songwe, Mkoa wetu wa Songwe ni mchanga ni mkoa wa kilimo, sisi tunashika nafasi ya tatu kwa uzalishaji wa chakula hapa Tanzania lakini pia tuna mazao ya biashara. Katika Mkoa ule ambao tunazalisha kwa kilimo, tunazalisha sana lakini tuna Shule za Msingi 193, Sekondari 64 katika vyote hivyo, shule zote hizo hakuna shule inayomuandaa kijana kwenda kuendeleza kilimo ambacho ndiyo wamekulia, ndiyo muhimili wa nchi yetu, uti wa mgongo. Sasa ina maana ile elimu wanayoipata, wanayosoma wote wale, inakwenda kusaidiaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu elimu haijagusa kwenye kilimo, ufugaji, uvuvi, haijagusa mambo yaliyopo katika ile jamii. Kwa hiyo, tunataka elimu tunayoipata iende kujibu maswali yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nimefurahi kusikia kwamba mnakwenda kuanzisha Vyuo vya Ufundi, na mimi nasema Mkoa wa Songwe tunahitaji Chuo cha Ufundi ili kiweze kusaidia sasa katika kuwapa ujuzi na maarifa ili iwasaidie katika kuendeleza katika mazingira yale ambayo tunayo. Kwa hiyo, naamini hilo mtalifanyia kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji vifaa vya kufundishia vya kisasa. Sasa hivi shule zetu zote ili ziweze kutoa elimu nzuri, zinahitaji kuwa na kompyuta TEHAMA, ziwe na vifaa vya kufundishia, ziwe na photocopy, hizi shule za kusema kwamba eti bila ya kuwaandalia mazoezi ya kutosha hatutaweza kufanya vizuri. Lakini mimi nataka kusema haya mambo mengine yote yamesemwa vizuri na waliotangulia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ninalotaka kulizungumzia ni udahili katika vyuo vya elimu ya juu. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongenza sana Mheshimiwa Rais kwa mambo mbalimbali anayoyafanya lakini ikiwemo ya kuanzisha ile filamu ya Royal Tour. Hii itatuletea watalii wengi. Baada ya watalii hao watakaokuja hapa nchini wengine watakuja kwa ajili ya kusoma. Tutakuwa na utalii wa shule, utalii wa kuja kusoma. Sasa kwetu hapa Tanzania tuna bahati ya pekee, Serikali mmejitahidi, Serikali lazima tuipongeze imejitahidi. Tuna Vyuo vya Elimu ya Juu zaidi ya 50, zaidi ya 50 Vyuo vya Elimu ya Juu viko hapa katika nchi yetu, nchi nyingi hazina hivyo vyuo. Tunayo mitaala mingi na mitaala yetu ambayo tunaitengeneza sasa hivi na nafurahi Mheshimiwa Profesa mnaipitia upya ile mitaala naamini mitaala mtakayokuja nayo itajibu mahitaji ya nchi yetu lakini lazima pia tuangalie mahitaji Afrika Mashariki, SADC, Afrika na tuangalie ulimwengu kwa ujumla kwamba wanahitaji nini hasa maana yake sisi ni sehemu ya ulimwengu, ni sehemu ya globalization. Kwa hiyo, lazima elimu tunayoitoa ikidhi mahitaji haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa basi ninachotaka kusema ni nini. Katika hivi vyuo vyote tulivyonavyo ambavyo vipo, sasa hivi mkakati Profesa uwe katika kudahili wanafunzi wengi wa hapa ndani lakini na wa nje. Tuchukue kutoka Kenya, Uganda, South Sudan, Ethiopia, Ulaya, wote mnaelewa Waheshimiwa Wabunge, UK ukiangalia pato lake la Taifa sehemu kubwa mchango wake wa Pato la Taifa unatokana na shule na watu mbalimbali wanapeleka kwenda kusomesha watoto kule na sisi tunataka sasa tufike mahali watoto waje kusoma hapa kwetu, nchi ya Tanzania tupo strategically located! Tutumie amani na utulivu kama tunu tuliyonayo hii ituletee sasa watalii wa elimu waje kusoma hapa na vyuo vyetu vipate wanafunzi wengi. Tukifanya hivyo, mitaala tukiiboresha, tukaondokana na haya mambo ya zamani!

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano Profesa zamani kulikuwa na mature age entry kwenye Vyuo Vikuu, tuliifuta tukaondoa. Sielewi kwa nini tuliondoa? Lazima tuiangalie hiyo kwa nini tuliindoa hivyo vitu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii watu wanasema mtu akitoka Kenya hana sifa ya kusoma kwenye Vyuo Vikuu vya kwetu, hivyo tunataka kusema sisi ndiyo tuna elimu nzuri kuliko hata ya Kenya? Hiyo siyo kweli, lazima hayo tuyaangalie! Kama kuna mahali tumefanya makosa ni kwenye eneo hilo. Tukaangalie udahili wetu tuanzishe mambo haya. Kama tunaona kwamba hawajakidhi vile vigezo vya kwetu anzisheni kozi ya foundation kwenye vyuo vyote, isiwe kwenye Open University tu, kwenye vyuo vyote, wapeni udahili wafanye foundation mwaka mmoja, wapate zile minimum qualification wasome hapa, walete dola nyingi, hizo dola zitatusaidia kwenda kulipa hata hii mikopo ambayo tunaikopa kwa ajili ya elimu yetu, tunakwenda kulipa. Sasa Tanzania tunasema tupo pazuri, pazuri bila kutumia hii nafasi tutashindwa. Kwa hiyo mimi nafikiri Mheshimiwa Profesa mtafanya mabadiliko makubwa na nimeona kwenye hotuba, nimeona kwenye mambo mengi na hatua ambazo mnachukua tunataka ziende zika-address haya zitusaidie kama nchi kuleta mambo tunayoyahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ina changamoto nyingi, watoto wengi wanakwenda kusoma wanakosa mikopo. Nafikiri ni wakati muafaka Profesa, hebu angaliaeni ni namna gani wadau mbalimbali wanaweza kuchangia kwenye hii Bodi ya Mikopo. Tupate fedha kutoka kwenye maeneo mengine tupanue wigo halafu watoto wetu wote wapate elimu, waweze kupata mikopo hiyo, wapate iwe ni kama vile vyuo vya elimu ya kati, Vyuo Vikuu wale wote wenye sifa wapate mkopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni mkopo watakwenda kulipa sasa kwa nini tuwanyime. Kwa hiyo, mimi nafikiri kwamba ni suala la msingi tuangalie hilo litatusaidia sana tukipanua wigo wadau wakachangia, tukawa na fedha za kutosha na tukaweza kufanya vizuri. Mimi naamini katika hatua hizo itachangia sana katika uchumi wa Taifa letu na nchi itaweza kupiga hatua vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo ninataka kusema ni ajira kwa wanataaluma. Wanataaluma kuna sifa zao, kuna vigezo na sisi kwenye ajira ndiyo tunataka huko tupanue ndiyo maana mimi nasisitiza sana hivi vyuo vyote tulivyonavyo tuajiri watu. Kwahiyo kwenye taaluma naomba Profesa aangalie.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo wameendelea kuifanya katika kuleta maeneleo ya nchi hii. Sote tunashuhudia Rais halali, usiku na mchana anahangaika huku na huko kutafuta rasilimali kwa ajili ya maendeleo ya nchi hii na maendeleo ya Watanzania. Nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Taasisi zake kwa kuja na mipango mizuri ambayo tumeisoma kwenye bajeti hii nzuri kabisa, bajeti ya mwaka 2023/2024, kwa kweli nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali pia kwa kuanza mchakato wa kuja na Dira Mpya ya Maendeleo ya kuanzia mwaka 2025 mpaka mwaka 2050. Dira iliyopo ambayo tulianza kuitekeleza mwaka 2000 mpaka 2025 ilikuwa na vipaumbele vitano ambavyo vilikuwa ni msingi wa kujenga nchi yetu. Kwanza ilikuwa ni kuboresha hali ya maisha ya Watanzania. Sote ni mashahidi miaka 25 sasa bado hali yetu haijawa vizuri sana, maisha ya Watanzania katika maeneo mengi bado hayajaimarika na hiyo inatupa fursa sasa kwamba tuangalie mikakati gani tunaiweka ili tuweze kuboresha maisha haya.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ilikuwa ni kuwepo kwa mazingira ya amani usalama na umoja ndani ya nchi yetu. Katika hili tumefanikiwa kwa kiwango kikubwa sana, hii ndiyo kigezo kikubwa cha kuiweka nchi yetu iwe tofauti na nchi zingine. Tatu ni kujenga utawala bora wenye uwajibikaji ufanisi na wenye tija. Nne, ilikuwa ni kujenga jamii iliyoeleimika na inayoendelea kujifunza na mwisho ni kujenga uchumi imara wenye kuweza kushindana na uchumi wa dunia yaani uwezo wa kukabiliana na ushindani.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika hali hiyo malengo hayo ni mazuri na ninaamini hata katika dira mpya itakayokuja itazingatia haya ambayo tumeyatekeleza yale ambayo tutakuwa hatujafanikiwa basi inaweza ikayapeleka kuyaweka katika dira inayokuja mpya ili tuweze kufikia miaka 50 Tanzania iwe ni nchi tofauti.

Mheshimiwa Spika, yapo mambo kadhaa ambayo ningependa kuchangia, lakini kwa leo nitachangia suala moja nalo ni suala la ajira kwa Watanzania. Tatizo la ajira ni kubwa katika nchi yetu, ajira ni haki ya kila mtu, na tunaposema ajira, iwe ni ajira ya kuajiriwa Serikalini pamoja na Taasisi zake, iwe ni ajira ya kuajiriwa kwenye kampuni binafsi na makampuni yao, iwe ni ajira ya kujiajiri ni haki ya kila Mtanzania kuifanya hiyo, hiyo ndiyo itakayoleta mchango mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukua Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Ibara ya 11(1) inasema; Mamlaka ya nchi itaweka utaratibu unaofaa kwa ajili ya kufanikisha utekelezaji wa haki ya mtu kufanya kazi, haki ya kujipatia elimu na haki ya kupata msaada kutoka kwa jamii wakati wa uzee, maradhi au hali ya ulemavu na katika hali nyingine za mtu kuwa hajiwezi na bila kuathiri haki hizo Mamlaka ya nchi itaweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba kila mtu anaishi kwa jasho lake.

Mhshimiwa Naibu Spika, kumbe hili suala la kufanya kazi ni haki ya Kikatiba, kila Mtanzania lazima afanye kazi. Ukisoma Ibara Ndogo ya Pili inasema kila mtu anayo haki ya kujieleimisha na kila raia atakuwa huru kutafuta elimu katika fani anayopenda hadi kufikia upeo wowote kulingana na ustahili na uwezo wake. Hii ni haki ya Kikatiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia maisha ya Watanzania sasa hivi wapo vijana wengi wamesoma katika vyuo vikuu, wamesoma katika vyuo vya kati, wana taaluma mbalimbali, wapo ambao hawajasoma lakini wote ni Watanzania. Wote wanatakiwa wapate ajira na ajira maana yake ni kufanyakazi. Sasa hivi ukienda mahali popote, ukienda huku Mijini wapo vijana wengi hawana kazi, hawafanyi kazi. Ukiienda kule vijijini vijana wengi hawafanyi kazi, TAIFA letu haliwezi kujengwa na watu kutokufanya kazi, lazima tuje na mkakati wa kuhakikisha ni wajibu wa Serikali kuratibu kwamba sasa watu wote wanafanya kazi na kila mtu tujue wewe unafanya kazi gani unachangia nini katika nchi, kila mtu lazima tujue na pale ambapo mtu hana kazi ni wajibu wa Serikali kuratibu na kumuonesha kwamba kuna fursa hizi kuna hii kuna hii, wewe unaweza kufanya kipi ili kila Mtanzania afanye kazi, kwa kufanya hivyo ndipo tutajenga uchumi imara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya umaskini wetu uliopo inatokana na Watanzania wengi kutokufanya kazi. Watanznaia wengi kutokuwa na ajira. Kutokuziona fikra, kutokuziona fursa za kufanya kazi, hii inaturudisha nyuma sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyakazi wa Tanzania wanaofanya kazi sekta ya umma bado maslahi yao siyo mazuri sana. Nina imani Serikali itaendelea kuboresha maslahi yao hawa wafanyakazi ili waweze kufanya kazi kwa weledi, kwa tija na kuleta ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wapo wafanyakazi wa sekta binafsi ambao tunawasahau, hawa wanalipwa viwango vidogo sana. Vile viwango wanavyolipwa haviwawezeshi kuishi, haviwawezeshi kujenga uchumi, haviwawezeshi kuwekeza, wala haviwawezeshi kulipa kodi. Kwa mantiki hiyo, hatuwezi kuondokana na umasikini kama hatutaweka nguvu katika hili kundi kubwa linalofanya kwenye sekta binafsi ambao viwango vyao ni vidogo. Huu ni wajibu wa Serikali kuratibu na kuangalia tufanye nini ili wapate maslahi mazuri ili walipwe vizuri waweze kufanikiwa. Hili litatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali, ili Watanzania walipe kodi, ili tujenge uchumi, ili tuwekeze; ukilipa vizuri zile hela ndiyo unawekeza na ndiyo unatoa ajira kwa watu mbalimbali. Hawa watu wote wakiwekeza kule, ndiyo ajira zitakuwa zimepatikana. Hatuwezi kuitegemea Serikali peke yake kuajiri watu wote, haitawezekana. Watanzania ni wengi, wote wanahitaji kufanya kazi. Ni wajibu wa Serikali kuratibu kwa mujibu wa Katiba yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufanikisha hili, tulitangaza vita vya ukombozi wa Afrika na tumefanikiwa kwa kiwango kikubwa, Tanzania ikiwa inaongoza ukombozi. Sasa ukombozi ule ulikuwa wa kuleta uhuru, sasa hivi tunahitaji ukombozi wa uchumi, na kubwa zaidi ni ukombozi wa fikra za Watanzania ili Watanzania hawa waone fursa na Serikali iwasaidie hizo fursa waweze kujenga uchumi imara.

Mheshimiwa Naibu Spika, bila sisi kufungua fikra zetu, bila sisi kufungua nchi hii yenye baraka, nchi hii ambayo ina ardhi nzuri yenye rutuba, ina madini, ina milima, ina maji, ina mbuga za Wanyama, ina kila kitu; Watanzania hatustahili kuwa masikini. Umasikini wetu lazima tukae chini tuone tunautatuaje ili nchi hii iweze kuwa ni yenye uchumi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka kusema, nchi yetu sasa hivi tutangaze vita ya kuja na ukombozi wa kifikra wa Watanzania ili tujenge uchumi wetu. Nchi yetu tunahitaji maendeleo ya watu, tunahitaji maendeleo ya nchi. Nami naamini, kama tutakaa chini na kutafakari haya, Tanzania itakuwa ni nchi bora katika Afrika na duniani. Moja, ni mahali pazuri pa kuishi; pili, ni mahali pazuri pa kufanya kazi; tatu, ni mahali pazuri pa kukaa; na Tanzania ni mahali pazuri pa kuwekeza. Tukijiona hivyo, nchi yetu itafanikiwa kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini dhamana hii Mheshimiwa Waziri Mkuu anayo, ataweza kuifanya vizuri kwa kushirikiana na Mawaziri, kwa kushirikiana na Serikali kwa ujumla, na kwa kushirikiana na Watanzania wote wenye uwezo, wenye weledi, wenye utaalamu wa kila namna, ili nchi hii tuisukume mbele tupate maendeleo, tuondokane na umasikini, tulete miradi ya maendeleo, tuwasaidie wananchi wa Vwawa, wananchi wa Tanzania, wananchi wa Mkoa wa Songwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata hii nafasi, nami niungane na wenzangu kwanza kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akifanya katika kutafuta rasilimali kwa ajili ya nchi yetu, pia katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maji. Ni kweli kabisa amefanya kazi kubwa sana na ndiyo maana tunaona miradi kila kona karibu kila Jimbo miradi mingi inaendelea. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na Watendaji wote wakiongozwa na Katibu Mkuu kwa kazi nzuri ambazo wamekuwa wakifanya, kwa kweli mnastahili kupewa sifa kwa sababu sote tunajua Wizara ya Maji tulikotoka, miradi ilikuwa ni miradi chechefu kweli kweli na ilikuwa ni miradi ambayo kwa kweli iliturudisha nyuma sana lakini sasa hivi kazi kubwa mmeifanya na sisi tunaona mwelekeo ni mzuri. Ninawapongeza sana kwa kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nimeona hata katika Jimbo langu mmenisaidia sana miradi. Kuna ule mradi mdogo ule wa Mlangali Mbewe pale unafanya vizuri, Mradi wa Itunga unafanya vizuri lakini kuna miradi mingine ya Msiya unaendelea kutekelezwa. Mheshimiwa Waziri nakubaliana na wewe kwamba maji ndiyo maisha. Maji ni uhai, maji ndiyo chakula chetu, maji ndiyo nishati, maji ndiyo usalama wa nchi na sote tunakubaliana na hayo. Kama hii ndiyo msingi kwamba maji ndiyo maisha yetu, ukiangalia nchi yetu ilivyo tumebahatika kuwa na mabonde, kuwa na mito, kuwa na maziwa makubwa, mpaka tunayo hata Bahari, sasa hatustahili kuendelea kulia kila siku kwamba tuna shida ya maji kwa ukubwa huu wa mambo yote haya ambayo tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachohitajika Mheshimiwa Waziri pamoja na kazi nzuri ambayo umeifanya, kilichobaki ni uje na mpango wa matumizi bora ya maji (water master plan) ya muda mrefu. Ukija na water master plan ya muda mrefu utakuwa umeacha legacy katika nchi hii. Sasa hivi tunatekeleza miradi mingi, kila mahali inatekelezwa lakini hatuwezi kuiendeleza nchi hii kwa kutekeleza hii miradi namna hii. Tuje na mpango ule wa maji namna ya kuyatumia yale maji, ili tutengeneze gridi za kuunganisha sasa kwamba hapa itatoka wapi, hapa itatoka wapi, hapa tutaunganishaje? Hiyo ndiyo itakuwa mpango wa muda mrefu wa kutatua tatizo la maji katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji yaliyoko katika nchi hii hatustahili kila Mkoa wala eneo lolote kukosekana kwa maji, kwa sababu tunayo mengi, tukiwa na gridi kubwa tukiwa na mpango huo wa matumizi basi kila kitu kitakwenda vizuri. Kwa hiyo, nadhani hili ni eneo ambalo unatakiwa uache legacy kubwa katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Waziri ulikuja kule Jimboni na wewe ni shahidi unaona Wilaya yetu ya Mbozi na Jimbo la Vwawa ambalo ni Makao Makuu ya Mkoa, upatikanaji wa maji ni chini ya asilimia 50. Sasa hivi maji katika eneo lile Mji wa Vwawa ni asilimia 49 wakati ndani ya nchi umesema upatikanaji wa maji umefikia asilimia 88.5 mijini. Mimi kwangu ni chini ya asilimia 50 Waziri na wewe ni shahidi ulikuja uliona. Kwa kweli hii haikubaliki!

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Wilaya inavyozalisha katika uchumi wa nchi hii, ukiangalia wananchi wanavyofanya kazi katika nchi hii, hatustahili kuwa na maji chini ya asilimia 50. Ulikuja tukazungumza miradi kadhaa tukaangalia mahali tutakakopata miradi miaka karibu mitatu tunazungumza hilo. Uliniambia tutachukua maji kutoka Ileje kwenye Mto Bupigu na mimi nikakwambia Mheshimiwa Waziri lazima tuwe na mkakati wa muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu na nikasema kule mnakosema uwe ni mkakati wa muda mrefu lakini nako inawezekana kuna changamoto na nikasema kuna maji yanapatikana kutoka kule Ilomba eneo la Mafumbo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ni mengi yangeweza kuchukuliwa kule kwa mserereko yakaja mpaka Nyimbili, yakaja Idiwili, yakaja Nyimbili yakafika mpaka Vwawa kwa njia ya mserereko. Pale tunahitaji fedha kidogo tu. Mheshimiwa Waziri hebu hili liangalie. Nisingependa kwamba niwe Mbunge wa kulialia humu ndani. Pale maji unatega tu maji yanaserereka mpaka Vwawa pale Mjini. Kwa kweli hili naomba mliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmekuja na mpango sasa hivi ule wa maji ya Momba, mimi nakubaliana nalo lakini ule hauji Vwawa sasa hivi. Mmesema unaishia Tunduma, kwa nini uishie Tunduma? Halafu mseme utakuja kwenda Mbozi na mpaka Vwawa mpaka Mlowo baadaye? Kwa nini msingetafuta hizo fedha mkaunganisha huu mradi ukatufikia mpaka maeneo yote ili na sisi tuweze kutatua tatizo la maji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri, nakuomba nakuomba kama Kaka yako hebu lifikirie Jimbo la Vwawa. Hebu iangalie Wilaya ya Mbozi, hebu iangalie Wilaya ya Mbozi mtupatie maji katika maeneo hayo ili tuondokane na changamoto za maji. Ipo Kata ya Nanyara, Kijiji cha Songwe, Lusungo na Songwe vina shida kubwa ya maji. Vina mradi wa maji wa mwaka 1978. Mradi ule ulikuwa ni mdogo mpaka leo hii kuna shida ya maji unatakiwa upanuliwe ukarabatiwe ili uweze kutosheleza mahitaji ya maji. Tunaomba hilo mlifanyie kazi na muone namna mtakavyoweza kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna Kijiji cha Ihowa, Kijiji cha Weru, Kijiji cha Shomora, Vijiji hivi vyote vinastahili kupata maji. Ije Igare kuna mradi mwingine ulikuwa mkubwa sana lakini maji hakuna. Mabomba yamepita maji hayajapatikana, maji hayapo. Sasa tunaomba mtufikirie muone namna mtakavyoweza kuboresha. Pale Vwawa, Ilolo tulichimba kisima, na wewe ulikuwa shahidi wakati ule ukiwa Naibu Waziri, tumechimba kisima. Kile kisima mmekuja kutuambia tena hakina maji mpaka leo. Sasa kama kisima tumewekeza tumechimba hakijapatikana maji, nini solution ya muda mrefu sasa? Sasa tunapataje maji maana tunahitaji haya maji. Kwa hiyo, nakuomba Mheshimiwa Waziri hebu jaribu kuangalia katika maeneo haya utusaidie hii miradi ya maji iweze kutatua matatizo yaliyoko katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Isango tunakushukuru sana mmeleta mradi wa kuchimba kisima ambacho kitasaidia sana kupunguza upatikanaji wa maji pale Kata ya Sanga lakini utakuja mpaka hapa Itengezya, nakushukuru kwa kazi hiyo inaendelea vizuri lakini tunaomba sasa itekelezwe mtuunganishe katika mradi mkubwa ili kusudi tatizo la maji la Wilaya ya Mbozi, Mji wa Vwawa, Jimbo la Vwawa mpaka hadi Mlowo liwe ni historia, utakuwa umeacha legacy kubwa nasi tutasema alikuwepo Waziri mdogo anaitwa Aweso akisaidiwa na Maryprisca walifanya kazi nzuri sana. Nakuomba Mheshimiwa Waziri tusaidie na sisi naamini tutakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia Mheshimiwa Waziri, maji ni uhai, maji ni usalama wa nchi, maji ni chakula, maji ni nishati. Tunahitaji uje na master plan ya matumizi ya maji. Uje na gridi, ikiunganisha nchi hii tuione miaka mitano, miaka 10, miaka 20, miaka 50 ijayo naamini utakuwa umefanya kazi nzuri na Mungu akubariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi. La kwanza, nianze kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakifanya katika kuwekeza katika miundombinu na maeneo mbalimbali. Tumeshuhudia namna uwekezaji ulivyo mkubwa kwenye kampuni yetu ya ndege, ndege mbalimbali zimenunuliwa na zingine ziko njiani zinakuja. Kwa kweli wamefanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia uwekezaji kwenye SGR ambayo ni matrilioni ya fedha. Tumeshuhudia uwekezaji kwenye bandari, kwenye upanuzi wa bandari na wametumia zaidi ya milioni 421 dola za Marekani kwenye upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam na maeneo mengine. Kazi kubwa wameifanya tunawapongeza sana. Kwa hiyo tunaipongeza Wizara, tunawapongeza watendaji wote, watendaji wa taasisi zilizo chini ya Wizara hii wanafanya kazi nzuri sana. Hongera sana sana kwa kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwanza kwa kutusaidia kuhakikisha kwamba Barabara ya Ruanda – Idiwili mapaka Nyimbili ikiwa inaelekea mpaka Itumba kwa kuiweka kwenye bajeti imepangiwa bilioni moja japo ni ndogo, lakini tumeona wameweka kilomita 21, tunawashukuru sana kwa kazi hiyo nzuri. Pia kuna Barabara ya Vwawa – Hasamba kwenda kwenye Kimondo, Kimondo cha aina yake ambayo wamekuwa wakiijenga, wanaendelea kuijenga. Tunaamini wataendelea kutenga fedha ili kuhakikisha kwamba ile barabara inakamilika, kusudi watalii wanapoenda kwenye kimondo waweze kufika kiurahisi. Tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna Barabara ya kutoka Ihanda kwenda Chindi kupitia Ipunga hii barabara wanaifanyia kazi, wanaihudumia, tunashukuru sana kwa wakiendelea kuihudumia. Kuna Barabara ya Hezya mpaka Itumba bado ilikuwa kwenye upembuzi yakinifu, sasa tunataka waikamilishe ili ile barabara sasa watu wa kutoka Malawi wanaweza wakapitia ile barabara mpaka kuja katika maeneo mengine, kwa hiyo tunaamini wataendelea kuifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Meneja wa Mkoa wa TANROADS, anafanya kazi nzuri sana. Huwezi kuamini wakati mwingine saa sita za usiku anakwambia naenda kuangalia sehemu fulani mkandarasi amekwama, naenda kufuatilia hiki, anafanya kazi nzuri sana na anatupa ushirikiano mzuri sana, nampa hongera kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi pale Mpemba tunaomba Bandari Kavu. Tunataka mizigo ikisafirishwa na TAZARA kutoka Dar es Salaam iende mpaka pale Mpemba ili Nchi za SADC, ziende kuchukulia mizigo pale itarahisisha sana na itakuwa imetoa mchango mkubwa sana tunaomba sana hilo liweze kufanyika na tunaamini litatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sanjari na hilo Reli ya TAZARA ni muhimu ikaimarishwa, ikaboreshwa, mabehewa yakatafutwa, uwekezaji ukafanyika, ile sheria tukaipitia upya ili kuhakikisha kwamba iendelee kutoa mchango mkubwa katika eneo la kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nchi yetu imebahatika kwa sababu ni nchi ambayo tuna bahari kubwa, tunayo Bahari ya Hindi, tunayo Maziwa na maeneo mengine. Nchi yoyote wenye bandari, yenye bahari haitakiwi kuwa maskini. Sisi tumebahatika kuwa na nchi ambayo tuna–access na bandari, sasa uwekezaji lazima ufanyike, natamani kuona Bandari ya Dar es Salaam ifanane na Bandari ya Rotterdam, Bandari ya Singapore na bandari zingine kubwa duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote yanawezekana kwa kuwekeza na uwekezaji wa kwenye bandari unaweza ukawekeza kwa hela ya kukopa, unaweza ukawekeza kwa kukopa kutoka kwa wananchi kama walivyofanya Wamisri, Wamisri wakati wanajenga ule mfereji wa Suez Canal wa pili wao walikopa kwa wananchi, wakaamua kujenga mfereji wa pili ili meli ziwe zinapishana, waliamua na sisi tunaweza tukawekeza pale kwenye bandari kwa hela ya kutoka kwa wananchi au tukakopa nje au tukafanya lolote lile maadam bandari yetu tuongeze uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali katika kuhakikisha bandari hii inapanuliwa, bandari hii ifanye kazi, tunataka kuona pale Bandari ya Rotterdam upana wa kule ni kilomita 42, sisi pale bado ni padogo. Kwa hiyo tunahitaji eneo hata lile lote la Kigamboni, watengeneze maeneo ya kuweka mizigo, waboreshe ili kusudi mizigo yote ya huku iweze kupitia pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo iwe tuna fedha iwe hatuna ambapo tumefanya maamuzi makubwa ya kukopa, ya kutafuta kila mahali tulivyowekeza na Bandari ya Bagamoyo atafutwe mwekezaji, ajenge na yenyewe ikiwezekana ile bandari nyingine kama itapatikana kokote tujenge ili tuweze kujenga uchumi imara wa nchi yetu. Tunaamini kwa kufanya hivyo, mizigo ya nchi jirani inaweza ikahudumiwa na nchi yetu ikapata fedha nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nakushukuru kwa kunipatia nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupewa nafasi. Niungane na wenzangu kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo wamefanya katika kuifufua Sekta hii ya Utalii ambayo ilikuwa imeathirika kwa kiwango kikubwa sana kutokana na Covid-19. Sote tunajua kwamba mwaka 2019/2020 watalii walishuka mpaka chini ya 600,000 lakini jitihada kubwa zimefanyika ambazo zimepelekea idadi ya watalii imeongezeka mpaka kufikia 1,500,000 mwaka 2021 na taarifa ya sasa hivi inaonesha wamefika milioni 3.8. Ni hatua kubwa Serikali wamefanya wakiongozwa na Rais wetu mpendwa mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kweli hongera sana kwa kazi hiyo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtalii ni nani? Mtalii ni mtu yeyote anayeweza kusafiri kutoka sehemu anakoishi akaenda sehemu nyingine kwa lengo la kupata burudani, kwa lengo la kwenda kujifunza, kwa malengo mengine. Unaenda sehemu nyingine kwenda kula Maisha, huo ndio utalii. Kwa hiyo tunahitaji tuwe na mikakati ya kuwawezesha watalii waka-enjoy, wakale maisha. Tunahitaji utalii wa wanyamapori, jitihadi lazima zifanyike idadi ya watalii wa wanyamapori iongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utalii wa milima pia uongezeke, nchi yetu ina milima mingi. Utalii wa miamba kama vile Olduvai Gorge lazima watalii waongezeke, tunayo miamba mingi nchi hii. Utalii wa mikutano mbalimbali inayofanyika katika nchi hii, lazima tuwekeze ili tuwe na mikutano ya aina mbalimbali kuvutia watalii. Tunahitaji utalii wa misitu, utalii wa matibabu, hospitali mbalimbali ambazo sasa hivi tunaboresha huduma tutapata watalii kutoka nchi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, tunahitaji vilevile watalii wa vyuo kuja kusoma na kuja kujifunza. Tunahitaji utalii wa fukwe na utalii wa mambo mengine mengi. Wote huu ni utalii, lakini maana ya utalii tunaupima kwa kuangalia idadi ya watu waliokuja wa ndani na wale wa kutoka nje, lakini na kiasi cha fedha killichoingia katika uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, ili tuweze kupata fedha za kutosha tunahitaji kuwekeza, lazima tuwekeze vya kutosha. Tuwekeze kwenye kujenga hoteli, kujenga kumbi za kitalii, kumbi zitakazovutia watu mbalimbali kuja kufanya mikutano hapa. Tunahitaji kuwekeza kwenye miundombinu, tunahitaji kuwekeza katika maeneo mbalimbali kuvutia watalii kutoka nchi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ili tufanikiwe tunahitaji kuboresha huduma. Sasa hivi huduma zetu katika meneo mengi ya utalii kwenye mahoteli bado hazijawa vizuri. Ni wajibu wa Wizara kuhakikisha inaboresha haya ili tuvutie watalii walio wengi. Tumeona kulikuwa na programu ile ya kuboresha utalii kusini ili kuhakikisha nchi yetu inapata katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na programu ya REGROW ambayo ilikuwa na dola za Marekani 150. Toka wakati ule mpaka leo ile programu bado haijafanikiwa. Kule kusini hatujatangaza ipasavyo vivutio na maliasili tulizonazo. Kule Mbozi tuna kimondo kizuri, hapo Iringa tuna Ruaha, tuna Mikumi, tuna Rungwe tuna milima, tuna wanyama, tuna kila aina ya vivutio. Lazima tuwekeze ili tuhakikishe kwa kweli na huko zinapatikana fedha zitakazotoa mchango mkubwa katika kuijenga nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kuna Ruaha kule, kuna maeneo mengine Rungwe kule kuna mlima na kuna kamto fulani kamuhimu sana, kana historia nzuri sana, kuna utamaduni. Kwa utajiri mkubwa huu tulionao nchi yetu tunahitaji kuwekeza. Tukiwekeza sekta zikajipanga vizuri nchi hii tutapiga hatua kubwa na tutapata maendeleo makubwa sana. Kwa hiyo, kazi ya Wizara ni kuhakikisha ina-coordinate sekta zote hizi tuwekeze. Tufanye kazi kwa pamoja ili nchi iende mbele na sisi tuone manufaa ya kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, tunahitaji kuwekeza zaidi, angalia royal tour. Tumetangaza kwa royal tour imeleta impact, je, tukitangaza? Sasa Wizara wajiongeze basi, waende sasa wakatangaze na maeneo mengine. Royal tour ni moja, je, maeneo mengine tumeyatangazaje? Mheshimiwa Rais ametuonesha mfano, sasa na wao wachukue pale alipoishia twende mbele tutangaze nchi hii tufanikiwe. Nina imani tutafanikiwa sana na tutafika mahali pazuri.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, tunaomba Wakala wa Misitu ibadilishwe iwe sasa ni Mamlaka ya Kusimamia Misitu yote Nchini. Misitu ni uhai, misitu ni maisha, misitu ni maisha yetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya, niwapongeze pia Watendaji wote wa Wizara na taasisi zote zilizoko chini ya Wizara ya Fedha na Mipango, wanafanya kazi vizuri na sisi sote tunaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya Wizara ya Fedha ni kubwa na wao wenyewe wameidadavua katika ripoti yao katika taarifa ambayo wamewasilisha ni nyingi na ni kubwa na wanafanya vizuri, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo mambo kama mawili au matatu ambayo nitajaribu kuzungumzia kwa kifupi. Jambo la kwanza nataka nianzie kwenye eneo la bima. Bima, kuna bima ya lazima na kuna bima za hiyari. Hasa kwenye eneo la bima hapa, katika nchi yetu yapo magari ya Serikali hayana bima, yapo majengo ya Serikali hayana bima, yapo majengo ya kibiashara hayana bima, matokeo yake ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi ajali nyingi zinazotokea barabarani nyingine nyingi zinasababishwa na madereva wanaoendesha magari ya Serikali. Sasa matokeo yake magari yale yanawagonga watu, yanagonga mali za watu binafsi, yanasababisha hasara kubwa. Kwa utaratibu wa nchi zote gari ikikugonga au ikagonga mali au ikaleta hasara yoyote, yule anayepata hasara anatakiwa afidiwe na bima. Kwa utaratibu wa sasa hivi wa magari ya Serikali ambayo hayana bima maana yake nini? Wale wanaogongwa wanapata hasara hawana mahali pakujitetea wala pakuomba fidia. Sasa hili siyo zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Serikali zetu mbili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar. Zanzibar wameliona na wamerekebisha sheria, magari yao yote ya Serikali yanalipa bima ya lazima ili yakisababisha hasara watu waweze kufidiwa. Tanzania Bara bado, sisi huku bado. Nadhani umefika wakati tuangalie hili, watu wanaathirika, watu wanaumia, watu wanapata majanga mengi na hakuna fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi tumeshuhudia kwenye jengo la kibiashara la hifadhi ya jamii pale Dar es Salaam, lift imedondoka na watu wamekwenda mpaka chini wameumia, hawana mahali pa kuomba fidia! Sasa hili lazima Wizara ilitazame na ione kwamba kuna haja ya kuja na mfumo wa kuhakikisha kwamba magari yote ya Serikali, majengo ya kibiashara na mengine yote yaweze kupata bima ya lazima ili kujikinga na majanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana Mheshimiwa Waziri ulifanya kazi nzuri na tulikupongeza kabisa. Mwaka jana katika Bunge hili, aya ya 113 kwenye Sheria ya Bima Sura 394 ulisema hivi: “Napendekeza kufanya marekebisho kwenye Sheria ya Bima kwa kuongeza wigo wa bima ya lazima (mandatory insurance) kwa kujumuisha masoko ya umma, majengo ya biashara, bidhaa zote zinazoingizwa kutoka nje, vyombo vya baharini na vivuko. Hatua hii ina malengo ya kuimarisha ushirikishwaji wa kifedha (financial inclusion) na kuleta matumizi sawia ya bima”. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hili ulileta zuri tukakupongeza Mheshimiwa Waziri, toka Financial Bill ile imepitishwa mwaka jana mpaka leo hii hamjaanza kuifanyia kazi, Kanuni bado hazijatoka kwa nini? Sasa kazi tuliyoifanya mwaka jana mpaka sasa hivi bado hamjaleta Kanuni! Sasa Kanuni hizi tungependa Mheshimiwa Waziri mzilete mzifanyie kazi. Mwaka umemalizika maana yake hii Sheria haijaanza kufanya hii kazi, kwa hiyo, ni vizuri mkaifanyia kazi, ikaanza kufanyakazi ili sasa ndiyo pale nasema tuongeze magari yote ya umma yanayosababisha ajali barabarani yawe na bima ya lazima ili nayo hiyo sasa wananchi waweze kunufaika, ile hasara wanayoipata waweze kufidiwa. Kwa hiyo, hili ni suala ambalo mimi nimeona ni la msingi sana na ni muhimu mkalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo ningependa Wizara ya Fedha mlifanyie kazi, ni kuiangalia upya Sheria ya Fedha za Umma Sura 348. Sheria ile Mheshimiwa Waziri ilitungwa mwaka 2011 na kuna marekebisho kadhaa yamefanyika mpaka mwaka 2020. Marekebisho yale yote ukiyaangalia Sheria ile inasema, lengo la Sheria ni kuleta usimamizi mzuri wa makusanyo na matumizi ya fedha za umma na kulipa Bunge madaraka ya kusimamia fedha za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, sasa tulipofika sasa hivi ukiitafsiri maana ya ile ni kwamba inazungumzia cash budget, inazungumzia fedha taslim. Sasa, sasa hivi uwanja mpana tunaouzungumzia kwenye usimamizi wa fedha za umma, tunazungumzia kwa mapana (financial management) siyo cash financial management. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, financial management ni zaidi ya hii sheria hii inavyosema. Financial management kwangu mimi ninavyoona Sheria hii sasa tuiongezee meno, tuiongezee upana, tuitazame upya ili sasa financial management iwe ndiyo msingi wa hii sheria ambayo tunaizungumzia ya mwaka 2001. Maana yake sasa miaka 23 imeshapitwa na wakati ni wazi mambo mengi yamebadilika. Kwa hiyo, sheria hiyo inatakiwa iangalie uandaaji na usimamizi wa bajeti ya nchi, hii sheria inatakiwa iseme. Pia sheria hii inatakiwa iseme usimamizi wa mapato na matumizi ambayo ndiyo inasema sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii inatakiwa inagalie mipango ya kodi mbalimbali na usimamizi wa mali zake, hii sheria lazima iseme. Sheria hii inatakiwa pia kubainisha na kuangalia namna tutakavyoitumia katika kudhibiti hali ya baadae (forecasting) tuta–forecast mambo mbalimbali yanayojitokeza kwenye dunia. Mabadiliko mbalimbali yanayojitokeza hii sheria inatakiwa iwe ndiyo msingi wa kuweza ku – forecast kuangalia nini tunatakiwa kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo kutafuta vyanzo vipya vya mapato, sheria inatakiwa ituoneshe, zaidi ya hapo kufanya maamuzi ya ushirikiano yaani kuangalia kama major na acquisition na mambo mengine mengi kama kuangalia madeni ya Taifa na mali za Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja lakini naamini Mheshimiwa Waziri ataenda kuiangalia hii sheria ili iwe ya muhimu zaidi, ahsante sana, nashukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2016
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia katika huu Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba niwapongeze Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kuleta marekebisho haya ya sheria hii ambayo imekuwa ni kikwazo kikubwa katika majukumu mbalimbali ya Serikali huko nyuma. Kwa kweli nawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kwanza niipongeze Serikali kwa kuamua kuleta vifungu vya kupunguza muda wa mchakato wa manunuzi. Tumekuwa tunatumia muda mrefu sana katika mchakato wa manunuzi. Na wakati mwingine katika baadhi ya taasisi kama huna wataalam, kama wale wa PMU hawajajiandaa inaweza ikafika mpaka mwisho wa mwaka bado mko kwenye mchakato wa manunuzi, kwa hiyo hii ya kupunguza muda, kwa kweli naipongeza sana Serikali ni kitu kizuri sana tulichokuwa tunakisubiri; hili ni suala la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nimefurahishwa sana katika muswada huu, ni hii ya kuiondoa wakala wa ununuzi wa bidhaa za umma yaani GPSA kuiondoa katika kupanga bei. Hili lilikuwa ni tatizo kubwa, GPSA ilikuwa inalalamikiwa kila mahali na bei ambazo zilikuwa zinawekwa katika mikataba zilikuwa ni kubwa sana haziendani na hali halisi. Sasa kuiondoa kwamba wasipange bei nadhani hii inakwenda vizuri sana na sheria ya sasa ambayo kwa marekebisho haya yanataka taasisi zitumie bei ya soko; kitu ambacho ni muhimu sana. Hii ilikuwa ni changamoto kubwa sana lazima tutumie bei ya soko, unakuta mfuko simenti unauzwa shilingi 15,000 bei ya soko, kwenye mikataba shilingi 20,000, 30,000 hii haikubaliki. Kwa hiyo marekebisho haya ni ya muhimu sana lazima tuyaunge mkono, mimi nafikiri ni suala la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na GPSA kuna tatizo lingine lipo TEMESA. TEMESA haijazungumzwa kwenye hii sheria nayo imekuwa ni matatizo kwenye utengenezaji wa magari na vipuri, bei ambazo zimekuwa zinawekwa na TEMESA ukienda mitaani ziko tofauti kabisa. Sasa hilo halikubaliki, lazima Serikali itazame hapo ifanye nini ili kuweza kurekebisha kusudi tuweze kutengeneza magari katika bei ambazo zinakubalika kwenye soko. Siyo zile ambazo zinawekwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho nilitaka kuchangia kwenye hii nimefurahishwa sana na hii sheria kwa kuleta sasa upendeleo maalum kwa kampuni za kizalendo, zinazomilikiwa na Watanzania. Hii ni suala la msingi sana kwa sababu mara nyingi kwenye upande wa construction makampuni mengi yaliyokuwa yanafanya kazi nyingi yalikuwa ni ya kigeni, na makampuni ya ndani yamekuwa hayapewi kazi kwa sababu ya kukosa mambo fulani fulani. Sasa hii ambayo imewekwa kwenye sheria ya kuwapa upendeleo wa makusudi, maalum nadhani ni suala la msingi sana ambalo limewekwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini haijaishia hapo na wataalam wa ndani kwamba tutumie wataalam wa ndani ili kuwajengea uwezo waweze kuchangia katika maendeleo ya nchi; hii nafikiri itatuletea maendeleo endelevu. Hatuwezi kuwa na maendeleo endelevu tukiendelea kutegemea wataalam kutoka nje, hatuwezi kuwa na maendeleo endelevu tukiendelea kutegemea makampuni yanayotoka nje, lazima tuyajengee uwezo makampuni ya ndani, haya ndio yatakayoweza kuleta maendeleo endelevu. Hili nafikiri ni suala la msingi sana ambalo naliunga mkono.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu ununuzi katika Serikali za Mitaa, tumekuwa na changamoto kubwa sana kwenye Serikali za Mitaa na huku ndio kuna matatizo mengi sana, mara nyingi kampuni nyingi ambazo zimekuwa zikifanya kazi kwenye Serikali za Mitaa zimekuwa zikiwa na matatizo mengi, nadhani kuna haja sasa ya kurekebisha vizuri, kulikuwa na kanuni zile zinazohusu manunuzi kwenye Serikali za Mitaa na kanuni za hii, mimi namwomba Mheshimiwa Waziri, hizi kanuni ziwe harmonized tuwe na kanuni moja inayo-apply sehemu zote; hizi kanuni ambazo mara nyingine ziko huku, nyingine huku zina toa loopholes kwa watu kutumia zile nafasi vibaya na kufanya fedha za umma zipotee kwa kiwango kikubwa. Hili ni suala la msingi ambalo lazima tulizingatie katika kuweza kuhakikisha kwamba mambo yetu haya yanakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kwenye Halmashauri kuna tatizo lingine, mimi nilikuwa nafikiri mwelekeo mzuri Halmashauri zingeshauriwa pale zinapoweza kununua baadhi ya vifaa zinunue zenyewe halafu zifanye kazi ziajiri vibarua wa kufanya kazi; ingekuwa ina maana sana. Mimi sielewi kwa nini ni lazima kama Halmashauri inaweza kununua grader kwa nini tumpe contractor, kwa nini sheria ilazimeshe kwamba lazima ipewe tender? Mimi nilikuwa nafikiri ni lazima sasa kama tuna grader tuajiri vibarua wa kuweza kufanya hizo kazi na tulime barabara kwa wingi hilo lingekuwa ni la msingi sana. Kwa hiyo ningeomba sheria iliangalie hilo, na ione namna gani tutakavyoweza kulitekeleza iatusaidia sana katika kuweza kusaidia kuleta maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi sheria ilivyo inataka kila kitu kiende kwenye tender hatuwezi kuweka kila kitu kiende kwenye tender, haiwezekani hilo ni la msingi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ambalo nilitaka kuchangia ambalo naliona sasa lilikuwa ni tatizo la mfumo huu wa ununuzi ni suala la bei, sheria ilikuwa imeweka kigezo kwamba bei huwezi uka-negotiate, huwezi uka-bargain bei ikapungua.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mtu ameweka bei za ajabu; nataka kweli afanye kazi au yupo peke yake au wapo wangapi kwa nini tusiruhusiwe, sheria hii sasa inaruhusu kuanza ka-bargain bei mimi ninadhani hili ndio suala la msingi sana, lazima tu-bargain bei, iendane na hali halisi pale tunapoona kwamba bidhaa ambazo mzabuni ameweka haziendani na hali halisi, tumwambie bei ya soko sio hiyo rekebisha kama unataka kazi na irekebishwe ili kazi ziweze kwenda na tuweze ku-save hela za umma na tuweze kupata thamani halisi ya fedha za umma.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ambalo ningependa nilichangie ni kuhusu value for money, ni kitu muhimu sana, haiwezekani katika hali ya kawaida mimi nikienda dukani nanunua kitu kwa shilingi 500 ukisema unatoka kwenye taasisi ya umma wanakwambia shilingi 5,000 hii haikubaliki kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, haikubaliki kwa sababu; sababu nyingine ambazo wanazitoa nyingine zina maana lile suala la kusema kwamba eti malipo ya Serikalini yanachukua muda mrefu sana kwa hiyo zile bei zinakuwa na interest hii nadhani ni message inafika kwenye Serikali mliangalie hilo. Hakuna sababu ya kuchelewesha sana malipo walipwe kwa wakati na hili tuachane nalo. Lakini bei lazima tuzingatie bei ya soko na tuzingatie thamani halisi ya bidhaa tulizonunua, sasa hivi vitu vingi unakuta haviendani na hali halisi value for money haiwi-considered hasa hili ni tatizo kubwa ambalo ninaamini kabisa katika hii sheria ni muhimu sana ikalitekeleza na ikaliangalia, naamini Wizara wataliangalia kwa undani zaidi ili tuone ni namna gani tunaweza kulitatua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa nirudie kwenye lile suala la kanuni za ununuzi wa umma, kuna baadhi ya vipengele vilikuwa vinakinzana na sheria kuu.
Mheshimiwa Waziri naomba ukaviangalie vizuri vile vipengele vinavyokinzana, vipengele vingine vilikuwa vinaweka utaratibu huku tofauti unakuta kwenye kanuni zinakuwa ni tofauti. Hasa naomba hizi ukaziangalie vizuri ili ziwe harmonize ziendane na sheria inavyotaka. Lakini zaidi ya hapo hizi kanuni zisichelewe, sheria hii inatakiwa ianze kufanya kazi; mimi niliamini inaanza kufanya kazi tarehe 1 mwezi wa 7, kesho kutwa. Lakini sasa kama kanuni zitachelewa zitasababisha hii sheria iendee kutumika na tuzidi kuchelewa zaidi. (Makofi)
Kwa hiyo, nilikuwa naomba muliangalie hili muziharakishe hizi kanuni zije kwa wakati ili haya marekebisho ambayo yamepitishwa na hii sheria yaweze kufanya kazi ile ambayo tunaitarajia.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo napenda niseme naunga mkono hoja, nashukuru sana kwa kunipa nafasi.
Muswada wa Sheria ya Uthamini na Usajili wa Wathamini wa Mwaka 2016
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mawazo yangu machache juu ya sheria hii ambayo ni muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda niipongeze Serikali kwa kuleta muswada huu kwa wakati ambao ni muafaka. Naamini kabisa muswada huu utatupunguzia matatizo mengi sana ambayo yamekuwepo maeneo mengi katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza nijikite katika maeneo machache. Eneo la kwanza ambalo ningependa kulisemea ni kuhusu huyu Msajili ambaye anatajwa katika sheria hii. Nimeona muda wa Msajili huyu ambaye ametajwa kwamba atateuliwa na atapewa miaka mitatu na baadaye anaweza akateuliwa tena kwa kipindi cha miaka mitatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nadhani Msajili ndio mtendaji mkuu. Kipindi cha miaka mitatu ni kipindi kifupi sana. Bodi ina miaka mitatu, Msajili miaka mitatu. Sasa mara nyingi hapa kwa sababu Msajili ndio mtendaji, panaleta mvutano kidogo. Wakati mtakapokuwa mnafanya uteuzi wa Bodi tutajikuta hata Msajili mwingine tena atakuwa anateuliwa, kiasi kwamba mwendelezo wa ofisi utakuwa unakosekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nataka kushauri, kama inawezekana, Msajili angekuwa anateuliwa kwa kipindi cha miaka angalau minne au mitano. Hiyo ingesaidia kwamba wakati bodi inateuliwa lakini kunakuwa na Mtendaji ambaye tayari yuko pale na ofisi inaweza sasa ikawa na mwendelezo wa kuweza kutekeleza majukumu yake. Tumeona katika Bodi nyingi, Wasajili wanakuwa na muda mrefu kidogo, wanakuwa na miaka minne au mitano, hii inasaidia sana katika kuweza kuimarisha utendaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda kulizungumzia ambalo linaelezwa katika sheria hii ni hili suala ambalo sheria inamtaka Msajili kuwasilisha taarifa kwa Waziri kwa miezi mitatu na Waziri baadaye ataiwasilisha hiyo taarifa katika Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wasiwasi wangu ni kwamba taarifa ambayo atakuwa anaiwasilisha ambayo itawasilishwa na bodi hii miezi mitatu baada ya mwaka kumalizika, hiyo taarifa naamini itakuwa bado haijakaguliwa. Ili taarifa iweze kuwasilishwa hapa Bungeni ni vyema basi taarifa hiyo ikawa imekaguliwa na mtu mwingine ameiona, ameiangalia kwa undani na akaona hii taarifa sasa inafaa kabisa kuja kuwasilishwa Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naona kabisa hii taarifa ya miezi mitatu itakuwa ni taarifa ambayo ni unaudited na hivyo haitaweza kutoa picha halisi ya utendaji wa taasisi inayohusika au wa bodi yetu inayohusika. Kwa hiyo, napendekeza kwamba kwa utaratibu mzuri kabisa, inafaa taarifa hiyo iwe ni ile ambayo itatolewa labda ni miezi sita baada ya kufunga mwaka ambapo sasa hiyo taarifa itakuwa imekaguliwa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu; taarifa hiyo itakuwa sasa ni taarifa ya mwaka mzima ambayo itakuwa na majukumu mbalimbali ambayo yametekelezwa na hiyo Bodi pamoja na huyo Msajili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hiyo taarifa itakuwa sasa inakidhi mahitaji yetu ambayo tunayahitaji, kuliko hivi sasa ambapo taarifa yenyewe inakuwa ni ya miezi mitatu itakuwa bado haijakamilika kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilikuwa nataka kulizungumzia, zipo njia nyingi ambazo zinatumika katika kufanya uthamini. Njia hizi zinategemea na lengo hasa la uthamini ni nini. Lengo ni kupata mkopo, lengo ni kutoa fidia au lengo ni sababu gani? Zipo sababu nyingi.
Sasa nilikuwa nafikiri kwamba umefika wakati hizi njia ili kusiwe na migongano, Mthamini mmoja anaweza akaleta taarifa fulani halafu ikagongana na Mthamini mwingine, ni vyema basi tukawa tunachagua njia, zikaelezwa katika kanuni zitakazotolewa na Mheshimiwa Waziri, tukaeleza kama ni mkopo kwamba tutatumia kigezo fulani; tutatumia njia fulani kwa ajili ya kuthaminisha. Kama ni fidia, basi lazima tuainishe kwamba ni njia hii ambayo ndiyo inafaa zaidi, hivyo hii ndiyo itakayofaa kuweza kuthaminisha mali zilizoko katika eneo fulani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hiyo itatusaidia katika kupunguza migongano ambayo inaweza ikajitokeza kutokana na Wathaminishaji kuwa wawili au watatu ambao wote wana sifa lakini wanatoa ripoti zinazotofautiana. Nadhani ni muhimu sana tukaziangalia hizo njia ambazo tunazitumia katika kufanya hizo valuation.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna njia nyingi zimetajwa katika hii sheria na vigezo vingi vimetajwa, kama tutazingatia labda gharama za soko, kama tutazingatia soko, yaani mali hiyo ina thamani kiasi gani, yaani market value au tutazingatia gharama (cost recovery program) au historical cost na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa vigezo hivi viendane na sababu hasa ya kufanya uthamini. Naamini kabisa kama zikiendana na sababu ya kufanya uthamini, inaweza ikasaidia sana na inaweza ikapunguza migogoro ambayo imekuwa mingi sana katika hii sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nashukuru, naona kabisa kwamba hii sheria ni nzuri na ni sheria ambayo itaweza kukidhi mahitaji yetu, itasaidia sana kupunguza migogoro ambayo imekuwepo katika maeneo mengi sana.
Kwa hiyo, naomba itakapokuwa imepitishwa, basi Mheshimiwa Waziri mwiharakishe katika kuitangaza na kuhakikisha kwamba inaanza kutumika ili kusudi kule kwenye kanda na kwenye Halmashauri zetu ziweze kuanza kuitumia hii sheria na iweze kutatua matatizo ambayo yapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na hayo machache, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo, wa Mwaka 2016
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nichukue nafasi hii kwanza kuipongeza Serikali kwa kuja na Miswada hii miwili ambayo ni Miswada muhimu sana katika maendeleo ya nchi yetu. Tumeona kabisa katika Miswada hii taasisi hizi inaonekana zitafanya kazi ya kufanya utafiti katika masuala ya kilimo na masuala ya uvuvi lakini pia itadhibiti na kuratibu shughuli zote zinazohusiana na maeneo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Miswada imekuja kwa wakati muafaka, lakini naomba nichangie kwa maeneo machache. Nianze na maeneo ya jumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hii Miswada yote miwili na mambo ambayo yanaelezwa katika hii Miswada miwili ni mazuri sana. Nianze kwanza na ukubwa wa Bodi. Nimekuwa nikisema na tutaendelea kusema, kwamba Bodi hizi ni gharama kubwa kuziendesha; Bodi hizi zinatumia fedha ya walipa kodi; na Bodi hizi zikiwa kubwa kiasi hiki, ufanisi wake unakuwa ni mdogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona kwenye hii sheria imeandikwa Bodi itakuwa na wajumbe tisa, ukijumlisha na Mwenyekiti pamoja na Mkurugenzi wanakuwa 11. Hiyo Bodi ni kubwa sana. Bodi hizi zikiwa kubwa namna hii, zinatuletea matatizo. Zinaongeza gharama za uendeshaji kwenye Serikali. Kwa hiyo, naomba waliangalie upya, hakuna sababu yoyote Bodi kuwa kubwa kiasi hicho. Bodi nzuri zinakuwa na Wajumbe wanne na Mwenyekiti labda na Mkurugenzi, wanakuwa sita maximum; lakini Bodi ya Wajumbe 11, kidogo inanipa wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nimeona katika muundo wa hizi taasisi, ni taasisi za utafiti nakubali, lakini najua kabisa katika hizi taasisi, nyingi ikiwemo Chuo cha Kilimo Uyole na vingine vingi, vilikuwa pia vinafanya kazi ya kutoa wataalam wanaohusiana na masuala ya kilimo na masuala mbalimbali. Wataalam hawa wa mafunzo mbalimbali ambayo walikuwa wanayatoa yalikuwa yanatolewa halafu wanasajiliwa, yanatambulika katika nchi. Vyuo hivi vilikuwa vimesajiliwa na Baraza la Taifa la Vyuo vya Ufundi (NACTE) na hivyo mafunzo waliyokuwa wanayatoa, iwe ni katika Astashahada au katika Stashahada au katika ngazi nyingine yoyote ni mafunzo yaliyokuwa yanatambulika na bado ilikuwa ni kazi muhimu sana katika kuchangia kupatikana kwa wataalam katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika huu Muswada sijaona mahali ambapo wanagusa hizi kazi kwamba pamoja na kazi za utafiti, lakini pia vyuo hivi vitafanya kazi ya kuzalisha hawa wataalam ambao tunawahitaji sana katika haya maeneo. Kwa hiyo, nafikiri ni suala la kuliangalia pia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo, hizi taasisi ni nani atakayekuwa anazisimamia? Taasisi za Elimu ya Juu tunajua kwamba kuna TCU wanazisimamia; taasisi nyingine za mafunzo tunajua kuna NACTE wanazisajili, wanazisimamia. Hizi taasisi za utafiti, ni nani ambaye ni regulator wa hizi taasisi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama vitafuata muundo wa Baraza la Taifa la Vyuo vya Ufundi (NACTE) maana yake hata muundo wake lazima ufuate ule muundo ambao ulishapitishwa wa taasisi hizo. Ambapo kunakuwa na Director General au Mkuu wa Chuo, anakuwa na wasaidizi wake, inaeleweka kabisa na muundo upo wazi wazi. Sasa hii tunayoiweka kwenye hii taasisi moja naona kunakuwa; mmesema kutakuwa na Naibu Mkurugenzi Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu kuna Mkurugenzi Mkuu anateuliwa na Rais, Naibu Mkurugenzi Mkuu anateuliwa na Waziri, Wakurugenzi wanateuliwa na Bodi. Naona kama tunajaza mambo ambayo yataleta migongano mbele ya safari kiutendaji. Yatagonganisha tu! Mtu atashindwa kutekeleza majukumu yake anasema bwana kwa nini unaniambia hivi? Wewe umeteuliwa na Rais, nami nimeteuliwa na Waziri; inaleta migongano. Kwa nini huyu Naibu sasa asiteuliwe na Bodi? Kwa nini tuweke mpaka hadi aende kuteuliwa na Waziri? Mimi sioni sababu. Nafikiri hilo kuna haja ya kuliangalia vizuri ili muundo wao uwe ni mzuri na uendane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hata kwenye taasisi ya kilimo, nimeona hakuna Naibu, lakini naamini kabisa wale Wakurugenzi wanatosha kabisa na wale watakaosimamia vile vyuo ambavyo vimezungumziwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha 22 mpaka 25 kimetoa masharti kwa watafiti wote watakaofanya utafiti wa masuala ya kilimo, wote lazima wasajiliwe na hii taasisi. Pia miradi watakayokwenda kuifanyia utafiti lazima isajiliwe, ni kitu kizuri tu, sina matatizo, isipokuwa naangalia, wapo watu walikuwa wanafanya utafiti wa masuala ya kilimo, wapo wanafunzi wanaosoma kwenye vyuo vyetu wanafanya utafiti huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, sasa tunataka kusema kwamba, hawa vijana ambao wanasoma au mtu kama yupo shuleni anasoma na anasoma Ph.D kwenye haya masuala, ni lazima kwanza akapate kibali kwenye hii taasisi ndiyo aendelee na utafiti. Sasa hilo naliona kidogo kama linakinzana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiri kwamba kuna haja ya kuangalia vizuri hizi ili kusudi tunaposema kwamba kila utafiti lazima usimamiwe, nakubaliana, lakini kuwe na utaratibu unaoeleweka kwa wale ambao wapo kwenye mafunzo ili kusudi tuepukane na matatizo ambayo tumekuwa tukikutana nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa tumekuwa na matatizo mengi sana. Tumeona kwa mfano, mwaka jana na mwaka juzi kule kwetu ilitokea kule Mbeya, watu walikuwa kwenye utafiti, wamefanya utafiti, wamepata mbegu mbovu, mbegu mbaya, badala ya kuzitupa, wamepeleka sokoni, wamewauzia wananchi wetu. Wamenunua mbegu mbaya na hadi ikaharibu kabisa kilimo. Sasa hiki siyo kitu kizuri, kwa hiyo, ni suala la msingi ambalo lazima tuliangalie katika mtazamo huo wa kudhibiti mambo yanayoendana na hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Miswada hii haijaonesha namna tutakavyokuwa tunashirikiana na vyuo vingine kama Chuo Kikuu cha Kilimo. Kwenye huu Muswada haijataja tutakuwa tunashirikiana nao vipi? Wale wataalam ambao wapo kule, watashiriki vipi katika hii taasisi? Kwa hiyo, nafikiri kuna haja ya kuliangalia vizuri na hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nataka kuzungumzia kuhusu mapato. Katika taasisi yoyote kuna mapato yanayotokana na shughuli wanazozifanya, lakini pia kuna mapato ya ushauri na pia kuna mapato yanayotokana na utafiti, yaani funded research. Zile funded research nimeangalia katika vile vyanzo haijazungumzwa. Ule ushauri wa kitaalam watakaokuwa wanatoa, haujazungumzwa pale. Sasa nafikiri kwamba ni vyema wakaangalia ili kusudi viweze navyo kuwa ni sehemu ya mapato ya taasisi hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo sijafurahishwa nalo, nimeona kwenye taasisi hizi sheria inasema watarithi mali na madeni ya taasisi zilizokuwepo. Tunapoanzisha taasisi kama hizi, tukisema zirithi na madeni yaliyokuwepo kwenye vyuo hivyo, vitashindwa kusonga mbele. Hayo madeni Serikali ingeyachukua ili vikianza vianze fresh badala ya kurithi madeni. Hili sioni kama linakuja vizuri. Kwa hiyo, ni suala la kuliangalia vizuri badala ya kurithi na madeni ambayo yapo nafikiri tungekuwa na utaratibu mwingine ambao ungeweza kusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeona kwenye adhabu zinazotolewa katika utekelezaji wa hizi sheria. Adhabu hizi napendekeza ziangaliwe vizuri. Naona kuna adhabu unakuta kwamba wanasema fine ya fedha, shilingi milioni 20; kifungo ni mwaka mmoja, fine ya fedha shilingi milioni 10; kifungo, miezi sita. Nadhani hizi adhabu zingehuishwa; afadhali ingekuwa inasema labda mwaka mmoja mpaka miaka mitano au muda gani; hii ingetusaidia sana katika kuweza kuweka vizuri hizi taratibu ambazo nafikiri ni muhimu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niongelee pia kuhusu suala la utafiti. Umefika mahali ambapo Serikali lazima itenge fedha za kutosha kwa ajili ya kugharamia taasisi mbalimbali zitakazotoa mchango katika nchi yetu. Kila mwaka tumekuwa tukiimba kilimo ni uti wa mgongo, sijui uvuvi, sijui nini na nini; bila kutenga fedha za utafiti, tutakuwa tunaimba kila siku, tutakuwa tunapiga kelele bila sababu yoyote. Lazima fedha za kutosha zitengwe na tuweke kama ni kuwekeza. Kufanya utafiti ni kuwekeza na matokeo ya tafiti…
MWENYEKITI: Ahsante.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.4) wa Mwaka 2016
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru sana kwa kupata hii nafasi ili niweze kuchangia katika muswada huu ulioko mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimpongeze Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuleta muswada huu mzuri, muswada ambao unakwenda kutatua matatizo mengi ambayo yamekuwa yakiikabili nchi yetu, kwa kweli tunampongeza sana.
Pia naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria kwa jinsi ambavyo wamechambua muswada huu na maoni yake ambayo wameyatoa ili kuboresha muswada huu, na nadhani kwa kweli wamefanya kazi nzuri, hongereni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningependa nichangie maeneo machache, lakini la kwanza ambalo ningependa nianze nalo ni hili suala la mikopo yenye dhamana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkopo wowote duniani una masharti yake, mkopo wowote ambao mtu anahitaji au taasisi inahitaji una masharti ambayo lazima kigezo hicho kizingatiwe. Sasa kwenye nchi yetu, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua kwamba kuna Serikali mbili; Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na katika hilo, imeweka mipaka baadhi ya masuala ambayo yanashughulikiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na masuala ya fedha ni mojawapo ya suala la Muungano, kwa hiyo hili ni lazima lishughulikiwe na sheria za Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na matatizo kwa muda mrefu na kumekuwepo na malalamiko ya pande hizi mbili kwamba katika baadhi ya mikopo ambayo imekuwa ikitolewa imekuwa haizingatii sheria, imekuwa haizingatii masharti na kanuni za mikopo. Mimi naona hii Sheria inayoletwa mbele yetu sasa inakuja kutatua haya. Sasa hatuwezi kuzungumzia ya nyuma, tukasema miaka mingi imepita, aaa, sasa wakati umefika ndiyo maana sasa Serikali ya Awamu ya Tano inataka kutatua haya ili tuweze kusonga mbele, kwa hiyo mimi nadhani hii ni nia njema kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema taasisi yoyote ambayo inaomba mkopo wa aina yoyote; kumekuwepo na tabia ya taasisi nyingi katika nchi hii zimekuwa zikiomba mikopo na zinaomba dhamana ya Serikali lakini inapokuja kulipa zimekuwa zinasuasua hazilipi, sasa hii sheria inaboresha, sheria hii sasa inakuja kutatua haya matatizo. Inasema taasisi yoyote ambayo itakopa ambayo ina miradi ya maendeleo, maadamu miradi hiyo itakubalika, basi ikope lakini tuangalie wana uwezo wa kulipa? Kama hawana uwezo wasipewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sheria jinsi ilivyoweka mimi nakubaliana nayo kabisa kwamba lazima tuangalie uwezo wa kulipa wa taasisi yenyewe na taasisi ikionekana ina uwezo ndiyo ipewe mkopo, haina iwezo isipewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri hii sheria tena imeweka masharti magumu. Imeweka masharti kwamba kama taasisi itakopa na itashindwa kulipa, basi wale viongozi wachukuliwe hatua hii sheria ni nzuri sana, wachuliwe hatua kweli kwa sababu dawa ya kukopa ni kulipa. Huwezi ukasema unakopa halafu unakimbia kulipa, dawa ya deni ni kulipa na ndiyo maana tunasema, hata Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar sasa inaruhusiwa kukopa katika miradi ile ambayo inaona kwamba ina manufaa kwa nchi yao, lakini pia lazima tuzingatie uwezo wa Zanzibar wa kulipa hayo madeni, ndicho kinachoelezwa katika hii sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani wakope halafu wasilipe, kwa hiyo kama watakopa, sheria hii inawaruhusu lakini tunasema tuangalie balance sheet yao wana uwezo wa kulipa maana ni masuala ya Muungano? Sasa wasipolipa itakuja kuwa ni tatizo la Muungano. Ili lisiwe tatizo lazima tuangalie uwezo wao. Tukiona hiki wana uwezo tutawaruhusu wakope, walipe, waiendeleze Zanzibar hilo mimi sidhani kama lina tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo hili mimi naunga mkono kabisa Sheria hii ilivyokaa imekaa vizuri na Wazanzibar nadhani ni wakati muafaka sasa wataendelea vizuri, watafanya vizuri lakini tunawashauri wakope na walipe na watalipa kwa taratibu zilizopo, watalipa principle, watalipa na riba ile inayotakiwa. Hatutazidisha riba, riba iliyokubalika ndiyo hiyo hiyo walipe. Kwa hiyo, mimi nadhani sheria imekaa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ambalo ningependa nichangie ni suala marekebisho ya hii sheria inayohusu mikopo ya elimu ya juu
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la Mikopo ya Elimu ya Juu, hii sheria sasa imesema vijana wetu wanaosoma kwenye vyuo vya elimu ya juu kulikuwa na malalamiko mengi. Kulikuwa na mambo mengi ambayo yapo. Sheria hii sasa inarekebisha inasema; hata vijana sasa wenye diploma waruhusiwe kukopa mimi nadhai hii sheria ni nzuri sana ya kuiunga mkono. Maana yake tuna vijana ambao wana stashahada katika fani mbalimbali, kwa mfano; fani za afya, mafundi mchundo tunahitaji, hatuhitaji watu wawe na degree, tunahitaji hawa wote wapate elimu itakayotusaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapokwenda kuwa nchi ya viwanda hao ndio wanaohitajika kwenda kufanyakazi, sasa ili tuwapate lazima wapate mikopo. Kwa hiyo huu utaratibu mimi naomba niseme kwamba nauunga mkono kabisa, sheria hii irekebishwe, vijana wetu wale wote wenye stashahada wapate mikopo na ikiwezekana badala ya kusema fani fulani fulani, fani zote ziruhusiwe kukopa, maana ni mikopo, watalipa. Watalipa hawa, wakikopa watalipa. Kwa
hiyo, mimi nashauri kabisa kwamba hawa vijana ni wakati muafaka waangaliwe.
masharti yaliyowekwa kwenye mikopo; kuna haja ya kupitia. Tunaweza tukaweka kwa mfano katika hii fani ya stashahada tukasema mtu yoyote ambae ana-upper second and above au ana-first class, ana-upper second uruhusiwe kukopa badala ya kuwawekea kwenye taaluma kwamba taaluma fulani ndiyo wakope wengine wasikope. Wote waruhusiwe washindane ili kuwe na uwazi katika utoaji wa hii mikopo. Mimi nadhani hili litatusaidia sana katika kuweza kuleta maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa nichangie kidogo kuhusu misamaha ya kodi. Sheria hii imezungumzia juu ya misamaha ya kodi ambayo imekuwa ikitolewa na Waziri na imeweka utaratibu mzuri kwa jinsi Waziri anavyoweza kutoa misamaha ya kodi. Mimi nadhani hili limekuwa ni tatizo la muda mrefu sana. Nchi yetu tunashindwa kuendelea kwa sababu ya misamaha mingine isiyokuwa na tija, na niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano imepunguza sana misamaha ya kodi kwa kweli nawapongeza sana, imepunguza sana hii. Lakini tuendelee kuboresha kabisa ili misamaha ya kodi itakayokuwa inatolewa itolewe iwe ni ile yenye tija tu, iwe yenye tija tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hao wanaozungumzia Kuhusu Utaratibu, ndiyo maana sisi tumeshinda Kata 22 kati ya ngapi, tunawapongeza. Sisi tumeshashinda hapa tunazungumzia kuleta maendeleo, jinsi ya kuwatumikia Watanzania hayo Kuhusu Utaratibu…mimi nachangia. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Mweyekiti, mimi nadhani waangalie kitu cha kufanya haya mambo ni ya msingi, tunazungumzia maendeleo ya nchi hii. Kwa hiyo, misamaha ya kodi itakayokuwa inatolewa tuangalie wale wote wanao-qualify zile taasisi...
ile misamaha ya kodi iwe ni misamaha yenye manufaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti mimi nadhani haya ni masuala ya msingi sana ambayo sheria hii iliyoko mbele yetu inaenda kuyatatua, lazima sote tuiunge mkono kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nimalizie kwa kusema nawapongeza Wabunge wapya ambao wameteuliwa na ambao wameapa jana, washirikiane nasi katika kusukuma gurudumu la maendeleo. Nchi yetu hii wananchi wanahitaji maendeleo ya kweli na naomba tushirikiane tulete maendeleo, ahsanteni sana.
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Nchi kuhusiana na Umiliki wa Maliasili wa Mwaka 2017.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ili niwe wa kwanza kuchangia katika Miswada hii miwili. La kwanza, naomba nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kuja na Miswada hii miwili. Miswada hii ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu tulikuwa tuna sheria nyingi zinazotambua rasilimali zetu za Taifa, lakini hizi zilikuwa hazijaunganishwa. Kulikuwa na Sheria za Ardhi, kuna Sheria za misitu na sheria nyingi tu; lakini sasa Serikali imeamua kuja na Miswada ambayo tunazitambua kwa pamoja maliasili zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maliasili ambazo tunazizungumzia sasa hapa, hatuzungumzii tu madini, tunazungumzia udongo wote wa kila namna, tunazungumzia hewa, tunazungumzia maji, tunazungumzia milima yote, maziwa yote tuliyonayo, tunazungumzia viumbe vyote vyenye uhai na visivyokuwa na uhai, tunazungumzia kila kitu ambacho kiko katika nchi yetu. Tulikuwa hatuna sheria moja ambayo inatambua maliasili zote hizo ili tuweze kuzilinda kwa pamoja, sheria hii sasa imekuja kutambua vyote kwa pamoja. Hii ni hatua nzuri sana na tutapiga kasi sana katika maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hii Sheria ya Maliasili zetu hizi, imeweka misingi mizuri sana ambayo sasa sheria nyingine zinazohusu maeneo mbalimbali zitakuwa zinatungwa kwa kuzingatia hii Sheria muhimu. Nami niseme nawashukuru hata Wapinzani, ukiangalia hotuba yao, wanakubaliana na hizi sheria. Wanachobaki kusema, ni kwamba muda hautoshi, tumekimbia haraka; lakini wanakubaliana kwamba kuna matatizo ambayo lazima yawe addressed. Sasa hatuwezi kusubiri kwamba tuwe na muda wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeibiwa vya kutosha, maliasili zimepotea kwa muda mrefu, hatuwezi. Lazima wakati huu tunaanzia hapa, kama kutakuwa na upungufu tutaendelea kushughulikia kadri muda unavyoendelea. Leo hii tuseme tunasubiti eti tuwe na muda muafaka, muda muafaka upi? Huu ndiyo muda muafaka sasa wa kushughulikia rasilimali za Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii imeweka utaratibu mzuri sana katika kila namna. Kwanza wanasema, labda nizungumzie kwenye Sheria hii ya Madini. Wanasema, Serikali sasa itahakikisha kwamba inasimamia utafiti. Utafiti huu utatuwezesha kujua kwamba maliasili tulizonazo zina thamani ya kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba labda hapa nieleze kidogo, watu wengi wanafikiri uwekezaji kwenye madini, uwekezaji kwenye hizi rasilimali ni sawasawa na uwekezaji mwingine. Kuna utafauti mkubwa. Kwenye hii sekta tunachosema, Serikali ikiwekeza ikafanya utafiti inakwambia kwenye eneo lako hapa kuna utajiri wa kiasi fulani. Sasa ukishajua utajiri ulionao ndiyo anza kutafuta utaratibu sasa wa kuanza ku-extract kutoka kwenye hiyo mali uliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria zilizokuwepo zilikuwa hazina utaratibu mzuri. Mali ni zetu kila kitu ni chetu, eti kwa sababu mtu ana mtaji, ana vifaa vya kuchimba, anakuja anachukua mali zote, sisi tunabaki hatuna kitu. Kwa hiyo, sheria hii sasa inaweka utaratibu, inasema anayetaka kuja kuwekeza, tukishajua mali zetu ziko hivi, ndiyo maana tunasema sasa tunaanza kumiliki asilimia angalau kwanza 16; tunaanzia hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hiyo 16 ni ndogo, kwa sababu kama haya madini ni yetu, huyu mtu anakuja tu na mtaji kuchimba, utampaje zaidi? Tunachochimba kinatakiwa kwanza kiukweli kabisa tugawane nusu kwa nusu. Wewe njoo na mtaji, mimi nina mali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunachosema sasa, ukiangalia utaratibu huu ni kwamba hisa lazima ziwekwe kwetu, zitambuliwe na sisi tuwe nazo; utaratibu huu umetumika na nchi nyingi. Tumeona Ivory Coast wamefanya, wanamiliki free hold wanazo pale Ivory Coast; lakini tumeona pia Niger wanazo. Tunaona nchi nyingi wanao huu utaratibu wa namna hii na Afrika Kusini nao walipitia mikataba yao. Kwa hiyo, tunasema na sisi katika utaratibu huu tulionao, lazima na sisi sasa mali zetu tufaidike, ndio maana tunasema lazima wananchi tumiliki sasa, tutakuwa na hisa na tutakuwa tunafanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii Sheria inaweka utaratibu mzuri sana. Inasema sasa wananchi wote tutakuwa tunamiliki hisa kwenye hii makampuni na hisa zetu hizi kwa kuanzia zitakuwa zinasimamiwa na Serikali kupitia Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, aliyechaguliwa na wananchi wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alichaguliwa na wananchi ndiyo maana tunampa mamlaka kwamba hebu simamia kwa niaba yetu. Tutaendelea kuweka utaratibu mzuri na kuendelea kuitumia hiyo maliasili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii inaweka utaratibu mzuri sana; na ni Serikali ya Awamu ya Tano imeona hilo; nashangaa kama kuna mtu anaipinga. Wajibu, ukiangalia kwa mujibu wa mgawanyo wa majukumu kuna Serikali, kuna Bunge na kuna Mahakama. Kila chombo kina kazi yake. Serikali ya Awamu ya Tano inasema hivi, pamoja na kwamba ni wajibu wa Serikali kuingia kwenye mikataba, lakini pia mhimili wa Bunge upate nafasi pale unapoona ni muhimu upitie hiyo mikataba; hii sheria imeweka utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Sheria hizi sasa, baadhi ya mikataba tukiihitaji tutakuwa tunapata, tunapitia, tunaishauri Serikali, tunaielekeza maeneo ya kwenda kurekebisha. Sasa hatukuwa na sheria kama hiyo, Sheria hii imekuja na ni Awamu ya Tano imeweka huo utaratibu, ambao ni utaratibu mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii imeweka utaratibu kwamba kwenye mikataba inayohusu mali zetu, tunapoingia kwenye migogoro ya kutokuelewana na mwekezaji, basi Mahakama za kwetu za humu ndani kama mhimili mwingine, ndiyo utumike katika kutatua hii migogoro. Kwa nini tuchukue fedha nyingi; mabilioni ya mapesa tunaenda kupeleka nje kwenye mali ambazo ni za kwetu? Kwa hiyo, sheria hii imekataa na imesema kwamba sasa tutakuwa tunamaliza humu ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nitashangaa sana kama mtu mwenye akili timamu, mtu yoyote mwenye nia njema na maendeleo ya nchi hii, atakuwa anasema eti hapana, kukiwa na migogoro tupeleke huko. Huko wapi? Nadhani utaratibu uliwekwa sasa hivi ni utaratibu mzuri sana ambao unatupa madaraka ya kuweza kufanya vizuri na kuweza kuiendeleza nchi yetu na kupata faida kubwa inayotokana na rasilimali za nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hapa, nawaombeni Waheshimiwa Wabunge, hizi sheria ni nzuri. Hizi sheria tunaziwekea sasa msingi. Hakuna sheria ambayo inaweza ikawa hundred percent perfect; baadaye kama kuna upungufu tutaita tena, lakini lazima tuwe na mahali pa kuanzia. Kwa hali tuliyonayo ambayo tunataka hapa kazi na lazima tukimbie, hii ndiyo sheria tuliyokuwa tunaisubiri kwa muda mrefu. Naipongeza sana Serikali kwa kuja na hii sheria na nawaomba kila mtu aiunge mkono ili angalau tupate maendeleo ya kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi sheria pia zimeweka utaratibu mzuri, kwamba katika maeneo yale ambayo yatakuwa na wawekezaji, iwe sasa ni lazima kwa wawekezaji kuingia ile tunaita cooperate social responsibility, iwe ni wajibu wa kampuni, wakae na wananchi wa eneo lile waone ni maeneo gani wanatakiwa kupata huo msaada. Zamani ilikuwa ni hiyari, sasa siyo hiyari kwa mujibu wa sheria hii, itakuwa ni lazima sasa wananchi wanufaike na rasilimali zilizopo katika maeneo haya. Kwa hiyo, nadhani huu ni utaratibu mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba wenzangu hasa ambao wako upande wa pili wale wanaoanza kudai TV Live, tumedai sijui kilimo, huu siyo wakati wake. Hatuzungumzii kilimo wala TV Live leo, tunachozungumzia hapa ni rasilimali za Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na naunga mkono hoja za Serikali.
Muswada wa Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba ya Maliasili za Nchi wa Mwaka 2017.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ili niwe wa kwanza kuchangia katika Miswada hii miwili. La kwanza, naomba nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kuja na Miswada hii miwili. Miswada hii ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu tulikuwa tuna sheria nyingi zinazotambua rasilimali zetu za Taifa, lakini hizi zilikuwa hazijaunganishwa. Kulikuwa na Sheria za Ardhi, kuna Sheria za misitu na sheria nyingi tu; lakini sasa Serikali imeamua kuja na Miswada ambayo tunazitambua kwa pamoja maliasili zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maliasili ambazo tunazizungumzia sasa hapa, hatuzungumzii tu madini, tunazungumzia udongo wote wa kila namna, tunazungumzia hewa, tunazungumzia maji, tunazungumzia milima yote, maziwa yote tuliyonayo, tunazungumzia viumbe vyote vyenye uhai na visivyokuwa na uhai, tunazungumzia kila kitu ambacho kiko katika nchi yetu. Tulikuwa hatuna sheria moja ambayo inatambua maliasili zote hizo ili tuweze kuzilinda kwa pamoja, sheria hii sasa imekuja kutambua vyote kwa pamoja. Hii ni hatua nzuri sana na tutapiga kasi sana katika maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hii Sheria ya Maliasili zetu hizi, imeweka misingi mizuri sana ambayo sasa sheria nyingine zinazohusu maeneo mbalimbali zitakuwa zinatungwa kwa kuzingatia hii Sheria muhimu. Nami niseme nawashukuru hata Wapinzani, ukiangalia hotuba yao, wanakubaliana na hizi sheria. Wanachobaki kusema, ni kwamba muda hautoshi, tumekimbia haraka; lakini wanakubaliana kwamba kuna matatizo ambayo lazima yawe addressed. Sasa hatuwezi kusubiri kwamba tuwe na muda wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeibiwa vya kutosha, maliasili zimepotea kwa muda mrefu, hatuwezi. Lazima wakati huu tunaanzia hapa, kama kutakuwa na upungufu tutaendelea kushughulikia kadri muda unavyoendelea. Leo hii tuseme tunasubiti eti tuwe na muda muafaka, muda muafaka upi? Huu ndiyo muda muafaka sasa wa kushughulikia rasilimali za Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii imeweka utaratibu mzuri sana katika kila namna. Kwanza wanasema, labda nizungumzie kwenye Sheria hii ya Madini. Wanasema, Serikali sasa itahakikisha kwamba inasimamia utafiti. Utafiti huu utatuwezesha kujua kwamba maliasili tulizonazo zina thamani ya kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba labda hapa nieleze kidogo, watu wengi wanafikiri uwekezaji kwenye madini, uwekezaji kwenye hizi rasilimali ni sawasawa na uwekezaji mwingine. Kuna utafauti mkubwa. Kwenye hii sekta tunachosema, Serikali ikiwekeza ikafanya utafiti inakwambia kwenye eneo lako hapa kuna utajiri wa kiasi fulani. Sasa ukishajua utajiri ulionao ndiyo anza kutafuta utaratibu sasa wa kuanza ku-extract kutoka kwenye hiyo mali uliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria zilizokuwepo zilikuwa hazina utaratibu mzuri. Mali ni zetu kila kitu ni chetu, eti kwa sababu mtu ana mtaji, ana vifaa vya kuchimba, anakuja anachukua mali zote, sisi tunabaki hatuna kitu. Kwa hiyo, sheria hii sasa inaweka utaratibu, inasema anayetaka kuja kuwekeza, tukishajua mali zetu ziko hivi, ndiyo maana tunasema sasa tunaanza kumiliki asilimia angalau kwanza 16; tunaanzia hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hiyo 16 ni ndogo, kwa sababu kama haya madini ni yetu, huyu mtu anakuja tu na mtaji kuchimba, utampaje zaidi? Tunachochimba kinatakiwa kwanza kiukweli kabisa tugawane nusu kwa nusu. Wewe njoo na mtaji, mimi nina mali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunachosema sasa, ukiangalia utaratibu huu ni kwamba hisa lazima ziwekwe kwetu, zitambuliwe na sisi tuwe nazo; utaratibu huu umetumika na nchi nyingi. Tumeona Ivory Coast wamefanya, wanamiliki free hold wanazo pale Ivory Coast; lakini tumeona pia Niger wanazo. Tunaona nchi nyingi wanao huu utaratibu wa namna hii na Afrika Kusini nao walipitia mikataba yao. Kwa hiyo, tunasema na sisi katika utaratibu huu tulionao, lazima na sisi sasa mali zetu tufaidike, ndio maana tunasema lazima wananchi tumiliki sasa, tutakuwa na hisa na tutakuwa tunafanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii Sheria inaweka utaratibu mzuri sana. Inasema sasa wananchi wote tutakuwa tunamiliki hisa kwenye hii makampuni na hisa zetu hizi kwa kuanzia zitakuwa zinasimamiwa na Serikali kupitia Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, aliyechaguliwa na wananchi wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alichaguliwa na wananchi ndiyo maana tunampa mamlaka kwamba hebu simamia kwa niaba yetu. Tutaendelea kuweka utaratibu mzuri na kuendelea kuitumia hiyo maliasili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii inaweka utaratibu mzuri sana; na ni Serikali ya Awamu ya Tano imeona hilo; nashangaa kama kuna mtu anaipinga. Wajibu, ukiangalia kwa mujibu wa mgawanyo wa majukumu kuna Serikali, kuna Bunge na kuna Mahakama. Kila chombo kina kazi yake. Serikali ya Awamu ya Tano inasema hivi, pamoja na kwamba ni wajibu wa Serikali kuingia kwenye mikataba, lakini pia mhimili wa Bunge upate nafasi pale unapoona ni muhimu upitie hiyo mikataba; hii sheria imeweka utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Sheria hizi sasa, baadhi ya mikataba tukiihitaji tutakuwa tunapata, tunapitia, tunaishauri Serikali, tunaielekeza maeneo ya kwenda kurekebisha. Sasa hatukuwa na sheria kama hiyo, Sheria hii imekuja na ni Awamu ya Tano imeweka huo utaratibu, ambao ni utaratibu mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii imeweka utaratibu kwamba kwenye mikataba inayohusu mali zetu, tunapoingia kwenye migogoro ya kutokuelewana na mwekezaji, basi Mahakama za kwetu za humu ndani kama mhimili mwingine, ndiyo utumike katika kutatua hii migogoro. Kwa nini tuchukue fedha nyingi; mabilioni ya mapesa tunaenda kupeleka nje kwenye mali ambazo ni za kwetu? Kwa hiyo, sheria hii imekataa na imesema kwamba sasa tutakuwa tunamaliza humu ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nitashangaa sana kama mtu mwenye akili timamu, mtu yoyote mwenye nia njema na maendeleo ya nchi hii, atakuwa anasema eti hapana, kukiwa na migogoro tupeleke huko. Huko wapi? Nadhani utaratibu uliwekwa sasa hivi ni utaratibu mzuri sana ambao unatupa madaraka ya kuweza kufanya vizuri na kuweza kuiendeleza nchi yetu na kupata faida kubwa inayotokana na rasilimali za nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hapa, nawaombeni Waheshimiwa Wabunge, hizi sheria ni nzuri. Hizi sheria tunaziwekea sasa msingi. Hakuna sheria ambayo inaweza ikawa hundred percent perfect; baadaye kama kuna upungufu tutaita tena, lakini lazima tuwe na mahali pa kuanzia. Kwa hali tuliyonayo ambayo tunataka hapa kazi na lazima tukimbie, hii ndiyo sheria tuliyokuwa tunaisubiri kwa muda mrefu. Naipongeza sana Serikali kwa kuja na hii sheria na nawaomba kila mtu aiunge mkono ili angalau tupate maendeleo ya kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi sheria pia zimeweka utaratibu mzuri, kwamba katika maeneo yale ambayo yatakuwa na wawekezaji, iwe sasa ni lazima kwa wawekezaji kuingia ile tunaita cooperate social responsibility, iwe ni wajibu wa kampuni, wakae na wananchi wa eneo lile waone ni maeneo gani wanatakiwa kupata huo msaada. Zamani ilikuwa ni hiyari, sasa siyo hiyari kwa mujibu wa sheria hii, itakuwa ni lazima sasa wananchi wanufaike na rasilimali zilizopo katika maeneo haya. Kwa hiyo, nadhani huu ni utaratibu mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba wenzangu hasa ambao wako upande wa pili wale wanaoanza kudai TV Live, tumedai sijui kilimo, huu siyo wakati wake. Hatuzungumzii kilimo wala TV Live leo, tunachozungumzia hapa ni rasilimali za Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na naunga mkono hoja za Serikali.
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2017.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ili nami niweze kutoa mchango wangu katika Muswada huu wa Fedha wa mwaka 2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kuja na Muswada mzuri sana. Naipongeza Serikali kwa sababu wenzetu wa upande wa pili wamesema bajeti ya mwaka huu ni bajeti ya ajabu na wamesema maneno mengi. Nami nataka niseme kweli ni ya ajabu bajeti ya mwaka huu. Ni bajeti ya ajabu kwa sababu ni bajeti ambayo imesikia kilio cha Watanzania, ni bajeti ambayo imezingatia maoni ya Wabunge, maoni ya wananchi wote yaliyotolewa katika sehemu mbalimbali, ni bajeti inayokwenda kutatua matatizo ya nchi hii, ni bajeti ya ajabu kweli kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami naipongeza sana Serikali kwa usikivu wake. Ukisoma Muswada huu kwa asilimia 80 umezingatia sana maoni ya Kamati ya Bajeti, maoni ya Wabunge yamezingatiwa, ni mambo machache tu ambayo yamebaki ambayo bado tutaendelea kurekebisha kadri muda unavyoendelea. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali na nasema ni bajeti nzuri na Muswada ni mzuri, ni Muswada ambao umezingatia sana maoni yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia kuhusu mchango wa asilimia 15 wa mashirika ya umma. Kwa mujibu wa sheria tuliweka kwamba mashirika yote ya umma yachangie kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali asilimia 15. Hata hivyo, hatukuweka tahadhari kwamba wanapochangia ni utaratibu gani utumike katika kukokotoa kodi ya mapato, wakati yale mashirika yatakapokuwa yanatengeneza vitabu vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivi sasa ilivyo ule mchango ambao unatolewa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali wanapoenda kukokotoa kodi ya mapato (corporate tax) kwenye zile taasisi, mchango huu hauhesabiki kama sehemu ya gharama ya taasisi husika. Hivyo inasababisha mapato ya taasisi yaonekane ni makubwa kwa sababu hii inawekwa pembeni, halafu ndiyo wanapiga kodi ile corporate tax. Matokeo yake ni kwamba kunakuwa na double taxation.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili linaweza likatatuliwa administratively tu. Linaweza likatatuliwa kwa kurekebisha kipengele hicho kwenye yale mashirika ya umma na kufanya kwamba ule mchango unaokuwa umetangulia wa asilimia 15 uwe ni tax deductible utolewe iwe ni sehemu ya gharama ya yale mashirika kabla ya kufikia hatua ya kukokotoa kiasi kinachotakiwa kutozwa corporate tax. Hii itasaidia sana mashirika ya umma yaweze kuendelea kufanya kazi sawasawa na hivyo hakutakuwa na double taxation. Huo ni ushauri ambao naipatia Serikali safari nyingine waweze kuliangalia ili kusudi waweze kurekebisha kipengele hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naipongeza sana Serikali kwa jinsi ambavyo wamefafanua kuhusu property tax ambavyo itakuwa inatozwa. Kwenye sheria hii wamesema kwamba watakuwa wanatoza Halmashauri za Majiji, Manispaa na Halmashauri za Miji, naipongeza sana kwa kuondoa Halmashauri za Wilaya. Kodi hii ingeenda mpaka kwenye Halmashauri zile za Wilaya ingeleta matatizo au malalamiko mengi sana kule vijijini, lakini kwa kuziondoa zile Halmashauri za Wilaya imekaa vizuri sana, naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuongezea hapo napenda kushauri kwamba mfumo ule wa kulipa kodi uwe mzuri kabisa. Kwa kuwa wamesema tutakuwa tunatumia mtindo wa kielektroniki basi wauimarishe ili wananchi wapewe namba rasmi za kuweza kulipa moja kwa moja badala ya kuanza kuhangaika kupanga foleni na kusumbuka katika kuilipa hiyo property tax katika ofisi za TRA.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine katika hilo, naipongeza Serikali kwa kuzifutia shule za watu binafsi pamoja na vyuo baadhi ya kodi, kwa kweli wamesikia vilio vyao. Hili suala la property tax bado Serikali halijaliangalia sana, ningeomba nalo iliangalie kwa sababu shule binafsi zile ardhi zinamiliki kwa public use. Kwa kuwa zinamiliki kwa public use, ina maana hata yale malipo ya land rent yafuate misingi ya public use. Pia property tax kuchaji madarasa kwa kweli inakuwa siyo vizuri sana, nalo hilo mngeliangalia pengine linaweza likasaidia sana katika kupunguza malalamiko ya hizi shule binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda nilizungumzie ni kuhusu hii industrial sugar yaani sukari inayotumika viwandani. Naipongeza Serikali kwa utaratibu waliouweka na kwamba kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu sana ya hawa wanaotumia sukari hii. Kumekuwa na ucheleweshaji sana wa refund lakini sasa hivi Serikali kwa kuwa imeamua kuja na Escrow Account, nashauri wahakikishe kwamba hii account inafunguliwa haraka kusudi waweze kuhakikisha kwamba vile viwanda vinarejeshewe mapema kadri inavyowezekana kusudi viendelee na uzalishaji bila kuchelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivi sasa vile viwanda vinadai hela nyingi sana Serikalini jambo ambalo siyo suala zuri sana. Kwa hiyo, ni vizuri hii account ifunguliwe haraka waharakishiwe yale madai kusudi waweze kuondokana na hilo tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda nilizungumzie ni kuhusu wharfage ambayo tumesema kwa mujibu wa sheria hii sasa itakuwa inakusanywa na TRA. Kama TRA watakusanya nakubaliana kabisa lakini ningeomba nishauri labda pengine zile bidhaa za nje zote TRA wanaweza kukusanya bila tatizo lolote kwa sababu wana-calculate kutokana na value ya zile bidhaa lakini bidhaa za ndani (local goods), nafikiri hii wharfage pengine TRA itabidi washirikiane sana na bandari katika kuhakikisha wanatoza kwa usahihi maana kuna usumbufu na kuna vibandari vingi vidogo. Hii pengine itasababisha TRA wakashindwa sana kufanya kazi hiyo, basi wakishirikiana na bandari wanaweza wakakusanya vizuri zaidi na zote zikatumika na zikaingia katika huo mfuko kama tunavyokusudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo napenda kuipongeza Serikali ni hatua ambazo zimechukua katika kuhakikisha kwamba inapunguza kodi kwenye zile kodi za wawindaji wa kitalii, zile hunting blocks wamepunguza kodi mbalimbali, kwa kweli ni hatua nzuri sana ambazo zitasaidia hii sekta iweze kukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, bado VAT kwenye utalii haijaangaliwa, ni vizuri tukaifanyia utafiti, ni vizuri tukaiangalia kwa undani ili tuone madhara ambayo yanatokana na hii kodi ya utalii kusudi tuweze kuimarisha sekta hii na tuweze kupata mapato makubwa zaidi ili yaweze kusaidia katika kuleta maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kama nilivyosema Muswada huu ni mzuri sana na utatusaidia sana katika kuleta maendeleo ya nchi na naamini vilio na michango yetu yote imezingatiwa. Ndiyo maana wengine walikuwa wanalalamika wanasema mbona wameongeza sheria nyingi, sheria zimeongezeka baada ya Serikali kusikia vilio vya Wabunge. Baada ya kupata michango imebidi yale maeneo yote ambayo Wabunge wamechangia, yaingizwe katika Muswada huu ili kusudi Serikali iweze kwenda kutekeleza majukumu kwa kuzingatia maoni na ushauri uliotolewa na Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kazi hii imekuwa ni nzuri, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na nawapongeza sana Serikali, naomba tushikamane, twende tukafanye kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii.