Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. David Ernest Silinde (203 total)

MHE. BONIFACE M. GETERE aliuliza:-

Je, Serikali inachukua hatua gani endelevu za kuondoa tatizo sugu la upungufu wa madawati kwenye baadhi ya shule za msingi na sekondari nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kabla sijaanza kujibu swali namba moja la Mheshimiwa Mwita Getere, naomba kwa idhini yako nitoe shukrani kwanza kwa Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kushinda uchaguzi, lakini vilevile kuweza kuingia ndani ya Bunge. Pia kwa kipekee kabisa nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa imani kubwa ambayo amenionesha kwangu mpaka kuniteua kuwa Naibu Waziri katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo nahudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba nikishukuru chama changu Chama Cha Mapinduzi kwa imani yake kubwa ambayo wameionesha kwangu kwa kunipa nafasi ya kugombea na mwisho wa siku kunisaidia kampeni na kushinda kwa kishindo. Nakishukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kipekee kabisa niishukuru familia yangu. Mama yangu mzazi kwa kuwa nami katika kipindi chote mpaka kufikia hatua hii ambayo leo nimefikia…

SPIKA: Sasa majibu!

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mwita Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniface Mwita Getere, Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, changamoto ya wanafunzi kukosa madawati katika shule za msingi na sekondari imetokana na mwitikio mkubwa wa wazazi kuandikisha wanafunzi shuleni baada ya Serikali kuanzisha mpango wa utoaji wa elimu bila malipo ambapo idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa kwenye shule za msingi na sekondari umeongezeka maradufu.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa madawati ambapo mpaka sasa mwaka 2015 kulikuwa na madawati 3,024,311 na mpaka sasa hivi kufikia mwezi Septemba 2020 Serikali imeongeza madawati kufikia madawati 8,095,207 ambapo kumekuwa na ongezeko la madawati 5,070,899.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na upungufu wa madawati, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutenga fedha kwa ajili ya utengenezaji wa madawati kwenye miradi yote inayotengewa fedha za ukamilishaji wa vyumba vya madarasa kwa shule za msingi na sekondari na kuhamasisha wananchi na kuwashirikisha wadau na asasi mbalimbali katika utengenezaji wa madawati pamoja na kuendelea kutenga fedha ya matengenezo ya madawati kwenye Halmashauri kupitia mapato ya ndani. Nashukuru sana.
MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza:-

Je, ni lini Shule ya Sekondari Isike iliyopo katika Kata ya Igombe itafunguliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, Mbunge wa Ulyankulu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Shule ya Sekondari Isike ilijengwa katika makazi ya wakimbizi kwa lengo la kuhudumia wakimbizi na watoto wa jamii inayowazunguka. Mwaka 2012, Serikali ilitoa maelekezo kwa wakimbizi wote waliokuwa wanaishi katika Kambi ya Ulyankulu warejee kwa hiari nchini kwao. Katika kutekeleza agizo hilo, wakimbizi walirejea makwao na wachache waliomba uraia na kuendelea kuishi katika maeneo hayo, hivyo shule ilibaki na wanafunzi wachache sana.

Mheshimiwa Spika, Serikali iliamua kuwahamisha wanafunzi waliobaki na kuwapeleka katika Shule ya Sekondari Ulyankulu. Kwa kifupi, kufungwa kwa shule hiyo kulitokana na kuzingatia matumizi sahihi ya rasilimali watu, fedha na vifaa pamoja na mazingira salama na bora kwa wanafunzi kujifunzia.

Mheshimiwa Spika, hadi sasa wanafunzi wa eneo hilo wamepelekwa na kupangwa katika Shule ya Sekondari Ulyankulu. Serikali itafungua Shule ya Sekondari Isike kama itabainika kuna mahitaji. Ahsante sana.
MHE. JERRY W. SILAA Aliuliza:-

Je, Serikali imefikia hatua gani katika utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Mwendokasi awamu ya tatu toka Gongolamboto mpaka Kariakoo ambao umeainishwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020 – 2025?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerry William Silaa, Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka Jijini Dar es Salaam (DART) inaendelea na utekelezaji wa mradi wa mabasi yaendeayo haraka maarufu kama mwendokasi unaotekelezwa katika awamu sita katika barabara zote kuu Jijini Dar es Salaam zenye urefu wa kilometa 146.2.

Mheshimiwa Spika, awamu ya tatu ya mradi wa mabasi yaendayo haraka inatekelezwa katika barabara za Nyerere, Bibi Titi, Maktaba, Azikiwe na Uhuru kutoka katikati ya Jiji la Dar es Salaam hadi Gongolamboto zenye urefu wa kilometa 23.6 ikiunganishwa na awamu ya kwanza na ya pili ya mradi huu katika vituo vikuu vya mabasi ya Kariakoo, Gerezani na Kivukoni.

Mheshimiwa Spika, kazi inayoendelea sasa ni tathmini ya zabuni zilizowasilishwa ili kumpata mkandarasi atakayeanza kujenga awamu ya kwanza ya mradi, kwa maana ya Lot 1, inayohusisha ujenzi wa barabara, kwa maana ya road works, vituo vidogo vya mabasi pamoja na kituo kikuu cha mabasi cha Gongolamboto.

Mheshimiwa Spika, zabuni ya kazi ya ujenzi awamu ya pili, inayojumuisha ujenzi wa karakana ya Gongolamboto, Kituo Kikuu cha Mabasi cha Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere pamoja na vituo mlisho vya Jet Club, Banana na Mombasa, zabuni yake haijatangazwa kutokana na mabadiliko ya usanifu wa karakana ya Gongolamboto baada ya eneo la karakana hiyo kubadilishwa kutokana na sehemu kubwa ya eneo la awali kuathiriwa na mradi wa reli ya kisasa.
MHE. KUNTI Y. MAJALA Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka walimu wa kike katika Shule za Msingi Birise na Donsee ambazo hazina walimu wa kike?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, asante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya ukosefu wa walimu wa kike katika Shule ya Msingi Birise na Donsee zilizopo katika Halmashauri ya Chemba, Mkoa wa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto hiyo Halmashauri ya Wilaya ya Chemba imempeleka mwalimu mmoja wa kike katika Shule ya Msingi Donsee wakati ikiendelea na utaratibu wa kukamilisha kumpeleka mwalimu mwingine wa kike katika Shule ya Msingi Birise.

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali ikijiandaa na mpango wa ajira na mgawanyo wa walimu wapya kwa Halmashauri zote nchini, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inazielekeza Halmashauri zote nchini kufanya msawazo wa walimu wa shule za msingi na sekondari kwa kuzingatia jinsia.
MHE. NAPE M. NNAUYE K.n.y. MHE. HASSAN S. MTENGA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza ruzuku katika mpango wa utoaji bure Elimu ya Sekondari na Msingi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutekeleza Mpango wa Elimumsingi Bila Malipo nchini ulioanza kutekelezwa mwezi Desemba, 2015. Fedha zinazotolewa kupitia mpango huo zinahusisha fidia ya ada, shughuli za uendeshaji wa shule, fedha za chakula kwa shule za bweni na malipo ya posho za madaraka kwa Wakuu wa Shule na Maafisa Elimu Kata.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali inaomba kutengewa kiasi cha shilingi bilioni
312.09 kwa ajili ya utekelezaji wa Mpango wa Elimu Bila Malipo ambalo ni ongezeko la shilingi bilioni 13.96 ikilinganishwa na shilingi bilioni 298.13 zilizoidhinishwa katika mwaka wa fedha 2020/2021. Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mpango wa Elimumsingi Bila Malipo kwa kadiri ya mahitaji na upatikanaji wa fedha. Aidha, kuanzia mwezi Desemba, 2015 hadi Februari mwaka 2021, Serikali imetoa kiasi cha shilingi trilioni 1.26 kwa ajili ya Elimumsingi Bila Malipo.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA Aliuliza:-

Je, Serikali inachukua hatua gani kumaliza tatizo la upungufu wa Walimu nchini, hasa shule zilizopo maeneo ya vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukabiliana na changamoto ya uhaba wa walimu katika shule za msingi na sekondari, kuanzia Disemba 2015 hadi Septemba 2020, Serikali imeajiri walimu 10,666 wa shule za msingi na walimu 7,515 wa shule za sekondari na kuwapanga kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa. Aidha, kuanzia mwezi Desemba 2015 hadi Septemba 2020, Halmashauri ya Mji Njombe imeajiri walimu 21 wa shule za msingi na walimu 111 wa shule za sekondari. Vilevile Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia itaajiri walimu wapya 6,000 wa shule za msingi na sekondari ifikapo Juni 2021 ili kujaza nafasi zilizoachwa na walimu waliofariki ama kustaafu kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, kupitia ofisi za wakuu wa mikoa imekuwa ikifanya uhamisho wa ndani kwa kuwahamisha walimu waliozidi hasa kwenye maeneo ya mijini na kuwapanga kwenye shule zenye uhaba mkubwa wa walimu ambazo nyingi zipo maeneo ya vijijini. Serikali itaendelea kuajiri na kuwapanga walimu kwenye shule za msingi na sekondari hasa zenye mahitaji makubwa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. DOROTHY G. KILAVE Aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa barabara ya Buza/Nzasa – Kilungule pamoja na daraja litamalizika hasa ikizingatiwa kuwa barabara hiyo inawaunganisha wananchi wa Temeke na Mbagala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais –TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy George Kilave Mbunge wa Jimbo la Temeke kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi unatekelezwa kupitia DMDP, Halmashauri ya Manispaa ya Temeke inatekeleza Mkataba wa ujenzi wa Barabara ya Nzasa – Kilungule – Buza yenye urefu wa kilometa 7.6. Kati ya hizo kilometa 5.4 zinajengwa kwa kiwango cha lami na kilometa 2.2 kwa kiwango cha zege; na ujenzi wa stendi ya mabasi Buza fungu namba 14 wenye thamani ya shilingi bilioni 19.13 bila VAT, chini ya Mkandarasi Mjenzi Group Six International Ltd. Fedha hizi ni Mkopo wa Serikali kutoka Benki ya Dunia na unaotekelezwa kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA).

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa mradi huu ulianza kutekelezwa tarehe 01 Aprili, 2020 na unatarajiwa kukamilika tarehe 30 Oktoba, 2021. Mpaka sasa ujenzi umefikia asilimia 69 na fedha kiasi cha shilingi bilioni 8.05 zimelipwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kufanya matengenezo ya miundombinu ya barabara za Jimbo la Temeke kulingana na upatikanaji wa fedha ili kuimarisha miundombinu ya usafiri na usafirishaji.
MHE. TARIMBA G. ABBAS Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kazi ya ujenzi wa mradi wa Mto Msimbazi ambao umetajwa katika Bajeti ya mwaka 2021/2022?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais –TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tarimba Gulam Abbas Mbunge wa Jimbo la kinondoni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali na Benki ya Dunia inatarajia kufanya majadiliano ya mapendekezo ya awali ya mradi mwezi Desemba 2021 na kusaini mkataba wa mkopo wa kiasi cha Dola za Kimarekani milioni 120 ifikapo mwezi Machi 2022 na utekelezaji wa mradi unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2022 baada ya kukamilisha masharti yote ya kutekeleza mradi.

Mheshimiwa Spika, huu ni mradi wa kukabiliana na mafuriko katika bonde la Mto Msimbazi. Mradi huo kwa sasa upo katika hatua za maandalizi ambapo usanifu wa miundombinu husika pamoja na nyaraka muhimu kwa ajili ya masuala ya mazingira na fidia zinaandaliwa.

Mheshimiwa Spika, Kimsingi mradi huu utahusisha pia ujenzi wa daraja jipya la Jangwani lenye urefu wa mita 390; Upanuzi wa mto kwa upande wa chini kuanzia barabara ya Kawawa hadi daraja la Salander ili kuruhusu maji ya mvua kwenda baharini kwa haraka;

Mheshimiwa Spika, Uimarishaji wa kingo za mto msimbazi katika maeneo korofi kwa upande wa juu katika maeneo ya Tabata na Kinyerezi ili kuzuia mmomonyoko wa udongo;

Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa vitega mchanga na vituo vya kuhudumia mto kwa ajili ya kupunguza kiwango cha mchanga kinachotuama eneo la chini la Mto Msimbazi;

Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa matuta kwa upande wa chini wa mto Msimbazi (kuanzia Daraja la Selander hadi Barabara ya Kawawa) yatakayoruhusu matumizi mbalimbali ya ardhi ikiwemo City Park eneo la Jangwani pamoja na maendeleo ya makazi maeneo ya Mchikichini, Sunna na Hananasif; Program za kuboresha usimamizi wa takangumu katika Kata 18 zinazozunguka bonde la Mto Msimbazi; na Kurudishia uoto wa asili katika maeneo yenye mikoko, maeneo yenye ardhi oevu, pamoja na misitu ya Pugu na Kazimzumbu, Wilayani Kisarawe.
MHE. ROBERT C. MABOTO Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano ya ujenzi wa barabara za lami katika Mji wa Bunda kwa kuwa mpaka sasa hauna barabara za lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Robert Chacha Maboto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji wa Bunda ina barabara za lami zenye urefu wa kilometa 2.22. Barabara hizi ni za Boma kilometa 1.36; Malugu kilometa 0.42; DC kilometa 0.24 na Posta kilometa 0.2. Barabara hizi zilijengwa kufuatia ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na mazungumzo na Benki ya Dunia kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Uendelezaji Miundombinu katika Miji (TACTIC) unaotarajiwa kutekelezwa katika Halmashauri za Majiji, Manispaa na Miji 45 ikiwemo Halmashauri ya Bunda Mji. Programu hii itahusisha pia ujenzi wa barabara za lami katika Mji wa Bunda kwa kuzingatia vipaumbele vitakavyoainishwa na Halmashauri ya Bunda Mji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itatekeleza ahadi zote za Rais zilizotolewa na aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano kama ilivyoahidiwa na Rais wa Awamu ya Sita Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan katika hotuba aliyotoa wakati akilihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 22 Aprili, 2021.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani kuwasaidia Wanafunzi ambao wamechaguliwa kwenda kusomea kozi ambazo hawakuzichagua katika Matokeo ya Mtihani wa Kidato cha nne yaliyotoka mwaka 2021?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais_TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Ranwell Mwenisongole, Mbunge wa Jimbo la Mbozi Kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali hutumia fomu maalum itwayo Student Selection Form (Sel-Form) ambayo humuwezesha mwanafunzi kuchagua tahasusi na kozi anazopenda kusomea endapo atachaguliwa kujiunga na kidato cha tano au vyuo vya ulimu wa ufundi, ambapo hujazwa na wahitimu wote wanaotarajia kuhitimu kidato cha nne mara baada ya kumaliza mitihani yao.

Mheshimiwa Spika, mwanafunzi anaweza kuchagua wapi anahitaji kwenda kusoma, kama ni kuendelea na masomo ya elimu ya Sekondari (kidato cha tano), vyuo vya elimu ya ufundi, vyuo vya ualimu au vyuo vya afya. Kwa kila chaguo mwanafunzi hupewa machaguo matano ya kuchagua tahasusi na shule anayohitaji kusoma au kozi na chuo anachohitaji kusoma. Endapo mwanafunzi ataridhia atapewa machaguo matano ya kozi na vyuo vya kati anavyohitaji kusoma. Wanafunzi huchaguliwa kujiunga na vyuo vya elimu ya ufundi, vyuo vya afya au ualimu endapo wamechagua kama chaguo la kwanza kwa sababu wanataka kupata ujuzi badala ya kujiunga na kidato cha tano au wamekosa nafasi ya kujiunga na kidato cha tano.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali haina mpango wa kuwagharamia wanafunzi wanaochaguliwa kusomea kozi mbalimbali katika vyuo vya kati isipokuwa wanafunzi wanaochaguliwa moja kwa moja kujiunga na vyuo vya ufundi vitatu ambavyo ni Taasisi ya Sayansi na Teknolojia Dar es Salaam (DIT), Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST).

Mheshimiwa Spika, Serikali imejikita kuongeza nafasi za kudahili wanafunzi wa kidato cha tano, hivyo idadi ya wanafunzi wanaojiunga na kidato cha tano imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka. Idadi ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano mwaka 2021 ni wanafunzi 87,663 ikilinganishwa na wanafunzi 73,113 waliochaguliwa mwaka 2020.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga vituo vya afya katika Kata za Tinginya, Muhimba, Kalulu, Mindu, Nalasi Magharibi na Nalasi Mashariki Wilayani Tunduru?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya katika ngazi zote nchini ikiwemo Wilaya ya Tunduru. Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2017 hadi 2020 Serikali imejenga na kukarabati Vituo vinne (4) vya Afya vya Mkasale, Matemanga, Mchoteka na Nakapanya Wilayani Tunduru kwa gharama ya shilingi biloni 1.5. Aidha, katika Mwaka wa Fedha 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 200 kwa ajili ya kukamilisha maboma manne (4) ya zahanati katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kwamba mahitaji ya vituo vya kutolea huduma za afya ni mengi nchini, ikiwemo Wilaya ya Tunduru. Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga na kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya nchini ikiwemo vituo vya afya kwenye Kata za Tinginya, Muhimba, Kalulu, Nalasi Magharibi na Nalasi Mashariki katika Wilaya ya Tunduru kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Hospitali ya Wilaya ya Urambo ilijengwa mwaka 1975.

(a) Je, Serikali iko tayari kuifanyia ukarabati wa majengo na miundombinu yake yote?

(b) Je, ni lini Serikali itabadilisha mashine ya X-ray ya Hospitali hiyo ambayo imepitwa na wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa Hospitali ya Halmashauri ya Urambo ni kongwe na kwamba Serikali itafanya tathmini ya hali ya uchakavu wa miundombinu ya hospitali hiyo ili kuona namna bora ya kufanya ukarabati au ujenzi wa hospitali mpya ya halmashauri hiyo. Aidha, katika mwaka 2015 hadi 2020 Serikali imetoa shilingi milioni 413 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Urambo. Ukarabati huo ulihusisha Wodi Maalum ya daraja la pili, ujenzi wa jengo la upasuaji, ukarabati wa mfumo wa maji taka pamoja na ukarabati wa Wodi ya Wanawake na jengo la wagonjwa wa nje na upo kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji/ ukamilishaji.

(b) Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa mashine ya X- ray iliyopo katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Urambo ni ya zamani . Ni vema Halmashauri ya Wilaya ya Urambo itoe kipaumbele na kutenga fedha kupitia mapato yake ya ndani ili kununua mashine ya kisasa ya X-ray. Aidha, Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, inasimamia utaratibu mpya wa Vifaa na Vifaa Tiba unaojulikana kama Managed Equipment Services (MES) kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD). Chini ya utaratibu huo, Halmashauri zinafungiwa mashine za X-ray, kupatiwa mafunzo kwa wataalam kuhusu matumizi na utunzaji wa mashine hizo, huduma ya kinga na ukarabati kwa vifaa tiba (Planned Preventive Maintenance) kwa muda wa miaka mitano. Gharama ya kununua mashine ya x-ray kwa fedha taslimu ni shilingi milioni 393.40. Endapo halmashauri itaamua kununua mashine hiyo kwa mkopo, italipa kidogo kidogo kiasi cha shilingi milioni 19.67 kila baada ya miezi mitatu kwa muda wa miaka mitano.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Barabara za kutoka Kata ya Kalenga kuelekea kata za Ulanda, Maboga, Wasa, Kihanga hadi Kijiji cha Mwambao ni mbovu sana: -

Je, ni lini Serikali itahakikisha barabara hizi zinapitika hata kwa kiwango cha changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2019/ 2020 Serikali kupitia TARURA katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ilichonga tuta la barabara lenye kilometa 25 iliyozinufaisha Kata za Maboga, Wasa na Kalenga kwa gharama ya Shilingi milioni153. Vile vile TARURA ilifanya matengenezo ya kawaida kwenye barabara ya Magubike, Igangindung’u yenye urefu wa kilomita nane iliyovinufaisha Vijiji vya Kihanga na Mwambao kwa gharama ya Shilingi milioni 69.17. Katika mwaka wa fedha 2021 barabara hizo zimetengewa kiasi cha Shilingi milioni 54 kwa ajili ya matengenezo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya barabara na madaraja nchi nzima kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-

Je, Serikali ipo tayari kuruhusu wananchi wanaoishi kwenye Miji ambayo ipo kando ya barabara kuu kama Mji wa Mafinga kufanya biashara kwa saa ishirini na nne?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kubuni mikakati mbalimbali katika kuwaendeleza wafanyabiashara wadogo ikiwa ni pamoja na kuwatengea maeneo kwa ajili ya kuendesha biashara zao na kuwatambua kwa kuwapatia vitambulisho vya wafanyabiashara wadogo na watoa huduma. Kutokana na uhaba wa maeneo ya kufanyia biashara kwenye baadhi ya Miji, yameanzishwa masoko ya usiku ambayo yanaendeshwa kwa kufunga baadhi ya Mitaa nyakati za jioni hadi usiku kwa ajili ya kupisha wafanyabiashara wadogo kuendesha biashara zao. Baadhi ya Halmashauri hizo ni Jiji la Dodoma, Jiji la Dar-es-Salaam na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji.

Mheshimiwa Spika, uendeshaji wa biashara nyakati za usiku umeonekana kuwa na changamoto nyingi za ulinzi na usalama wa wafanyabiashara, wateja pamoja na bidhaa zao. Uzoefu unaonesha kuwa maeneo zinakofanyika biashara kwa saa 24 kuna miundombinu yote muhimu ikiwemo taa, kamera, vyoo na maeneo ya kuhifadhia bidhaa za wafanyabiashara.

Aidha, ili kuwa na usalama wa uhakika katika masoko, kunahitajika ulinzi wa Polisi au Askari wa akiba kwa maana ya Mgambo, hususan nyakati za usiku. Serikali kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama itaendelea kutafuta namna bora ya kuwezesha wafanyabiashara waishio kwenye Miji kando ya barabara Kuu ikiwemo Mafinga kufanya biashara zao kwa saa 24 ikiwa ni pamoja na kuweka miundombinu ya msingi.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya kujaa maji mara tu mvua zinaponyesha katika baadhi ya maeneo ya Kata za Magomeni, Shangani, Ufukoni, Reli na Likombe katika Manispaa ya Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya kujaa maji mvua zinaponyesha katika baadhi ya maeneo ya Kata za Magomeni, Shangani, Ufukoni, Reli na Likombe katika Manispaa ya Mtwara Mikindani. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali kupitia Mradi wa Uendelezaji Miji (Tanzania Strategic Cities Projects) imejenga mifereji ya kutoa maji kwa maana ya stand-alone drains yenye urefu wa kilomita 10 kwa gharama ya shilingi bilioni 1.82 katika Kata za Shangani, Reli, Likombe na Vigaeni Manispaa ya Mtwara Mikindani.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kukamilisha Mpango Kabambe wa kuyaondoa maji ya mvua katika makazi na kuyaelekeza baharini katika Manispaa ya Mtwara Mikindani. Serikali itatafuta fedha ili kutekeleza kikamilifu Mpango Kabambe wa kuondoa maji ya mvua kwenye makazi na kuyaelekeza baharini katika Manispaa ya Mtwara Mikindani.
MHE. ASIA A. HALAMGA K.n.y. MHE. SAMWELI X. HHAYUMA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa stendi ya mabasi ya Mji wa Katesh?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Samweli Xaday Hhayuma Mbunge wa Hanang kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Hanang ni miongoni mwa mwa Halmashauri zilizokidhi vigezo vya kupatiwa fedha za ujenzi wa stendi ya mabasi kupitia Mpango wa Mradi Mkakati katika Halmashauri. Lengo la Serikali kuanzisha Mpango huu ni kuziwezesha Halmashauri kubuni miradi itakayoziongezea mapato ili kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Stendi ya Mabasi ya Katesh wenye gharama ya shilingi bilioni 5.60 ni miongoni mwa miradi 20 ya kimkakati nchini ambayo utekelezaji wake ulisitishwa katika mwaka wa fedha 2019/2020 kutokana na changamoto mbalimbali zilizojitokeza kwenye hatua za mwanzo za utekelezaji. Serikali ilizifanyia kazi changamoto hizo kupitia timu ya wataalam iliyoundwa na kutafuta namna bora ya kutekeleza miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, timu ilitoa maoni kadhaa yaliyotakiwa kutekelezwa na Halmashauri ya Hanang ikiwa ni pamoja na kupitia upya vipengele vyote vya mkataba, hususan muda wa mkataba na masharti ya dhamana ya awali kwa maana ya advanced payment guarantee. Hadi Machi, 2021 Halmashauri ya Wilaya ya Hanang imekamilisha taratibu zote kama ilivyoelekezwa na timu ya wataalam tayari kwa kuziwasilisha Wizara ya Fedha na Mipango. Hivyo, mradi utaendelea baada ya Wizara ya Fedha kupitia nyaraka hizo na kujiridhisha.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza:-

Je, ni lini barabara ya kutoka Kilando – Katete – Kazovu – Korongwe katika Wilaya ya Nkasi itakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa Rukwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabaraya Kirando – Korongwe ina urefu wa kilomita 35. Matengenezo ya barabara hii yalianza mwaka wa fedha 2017/2018 kwa kuanza na usanifu wa barabara yote ya kilomita 35 na usanifu wa daraja moja la mita 40 la Mto Kavunja; Usanifu wa madaraja mawili yenye urefu wa mita 12.6 kila moja.

Aidha, katika mwaka wa fedha 2016/2017, TARURA ilifungua Barabara ya Kirando – Kazovu yenye urefu wa kilomita 22 iliyotengenezwa kwa gharama ya shilingi milioni
108.37. Katika mwaka wa fedha 2021/2022, kiasi cha shilingi milioni 11.4 zitatengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara yenye urefu wa kilomita 11.4.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/ 2019, Serikali ilianza ujenzi wa daraja la Mto Kavunja lenye urefu wa mita 40 kwa gharama ya Shilingi bilioni 1.76 na shilingi milioni 954.70 zimeshapokelewa na ujenzi unaendelea ambapo daraja hili linatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2021. Vilevile, katika mwaka wa fedha 2021/2022, daraja hili litatengewa kiasi cha shilingi milioni 500.

Aidha, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara na madaraja yaliyobaki kwenye Barabara ya Kirando – Korongwe kulingana na upatikanaji wa fedha ili kuondoa changamoto ya usafiri kwa wananchi wa Kazovu, Kitete na Korongwe katika Wilaya ya Nkasi.
MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ya ujenzi wa barabara ya urefu wa kilomita tano kwa kiwango cha lami Wilayani Ikungi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imepanga kufanya usanifu na tathmini ya gharama za ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami katika Mji wa Ikungi. Utambuzi wa barabara hizi umekuwa shirikishi ili kutoa kipaumbele kwenye barabara zenye umuhimu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, hadi Machi, 2021, TARURA imetoa shilingi milioni 598.22, kati ya shilingi milioni 890.89 zilizotengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 97.92 katika ya Wilaya ya Ikungi. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali itaomba kuidhinishiwa shilingi milioni 925.08 kwa ajili ya matengenezo yenye urefu wa kilomita 92.6. Vilevile Shilingi bilioni 1.4 zitatengwa kwa ajili ya ujenzi wa daraja la Mihyuge Wilayani Ikungi.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kufanya usanifu na kujenga barabara kwa kiwango cha lami kwenye maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Ikungi kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itaongeza bajeti ya barabara za Newala Vijijini ambayo imetengewa fedha za kilometa 340 wakati zina mtandao wa barabara wa kilometa 960?

(b) Je, Serikali inatoa msaada gani wa dharula kwenye matengenezo ya barabara za vijijini vinavyozungukwa na milima au mito kama vile Mkongi – Nanganga, Mikumbi – Mpanyani, Namdimba – Chiwata, Mkoma – Chimenena na Miyuyu – Ndanda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maimuna Salum Mtanda, Mbunge wa Jimbo la Newala Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Newala ina mtandao wa barabara wenye urefu wa kilometa 960.04. Serikali imekuwa ikiongeza fedha za bajeti ya matengenezo ya barabara katika Halmashauri ya Newala mwaka hadi mwaka. Katika mwaka wa fedha 2019/2020, shilingi milioni 939.27 zilitengwa kwa ajili ya kuzifanyia matengenezo barabara zenye urefu wa kilometa 343.86, mwaka wa fedha 2020/2021, shilingi milioni 976.88 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 320.38.

Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi bilioni 1.056 kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 277.35 na ujenzi wa mifereji yenye urefu wa kilometa 1.37.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020 barabara ya Mkwiti - Lochino - Nyangao yenye urefu wa kilometa 11.1 imefanyiwa matengenezo kwa gharama ya shilingi milioni 84.78. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 barabara hii imetengewa shilingi milioni 56.32. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 87 kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Maputi – Mikumbi – Miyuyu – Ndanda Kibaoni yenye urefu wa kilometa 17.5 ikiwa sehemu ya kipande cha Mlima Miyuyu – Ndanda na shilingi milioni 56 kwa ajili ya matengenezo ya maeneo korofi yenye urefu wa kilometa 3.5 ili iweze kupitika hadi Kijiji cha Lochino.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015 ya ujenzi wa kiwango cha lami barabara yenye kilometa 13 kuanzia Rau Madukani – Mamboleo – Shimbwe Juu katika Jimbo la Moshi Vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Patrick Alois Ndakidemi, Mbunge wa Jimbo la Moshi Vijijini, kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza ahadi zilizotolewa na Waheshimiwa Marais walizozitoa katika Awamu zote. Katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 na 2019/ 2020 Serikali imeendelea kujenga kipande cha barabara chenye urefu wa mita 288 kwa kiwango cha lami kwa gharama ya shilingi milioni 190 kwa barabara ya Rau Madukani – Mamboleo - Shimbwe Juu. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, barabara hi iilifanyiwa matengenezo ya muda maalum yenye urefu wa kilometa 9 kwa kiwango cha changarawe ambayo iligharimu shilingi milioni 148.85. Vilevile katika mwaka wa fedha 2021/2022 barabara hii imetengewa bajeti ya shilingi milioni 10 kwa ajili ya matengenezo ya sehemu korofi yenye urefu wa kilometa 2.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea na ujenzi na matengenezo ya barabara nchini ikiwemo Moshi Vijijini kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. FELISTA D. NJAU aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua tatizo la mafuriko katika maeneo ya Mbweni Teta, Bunju Basihaya, Kunduchi, Nyamachabes, Ununio na Mikocheni katika Jimbo la Kawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Felista Deogratius Njau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya mafuriko katika maeneo ya Mbweni Teta, Bunju Basihaya, Kunduchi, Nyamachabes, Ununio na Mikocheni katika Jimbo la kawe. Serikali kupitia Mradi wa kuboresha Miundombinu katika Jiji la Dar es Salaam (DMDP) imetenga shilingi bilioni 8.4 kwa ajili ya ujenzi wa mfereji wa maji ya mvua wenye urefu wa kilomita 8.89 katika Kata ya Mbweni. Awamu ya pili ya mradi huu itajumuisha mifereji ya maji ya mvua katika maeneo ya Kunduchi, Nyamachabes, Ununio na Mikocheni.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya barabara, madaraja na mifereji ya maji ya mvua ili kuondoa kero ya mafuriko katika maeneo mbalimbali Jijini Dar es Salaam ikiwemo Jimbo la Kawe.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA aliuliza:-

Mwaka 2015 wakati wa Kampeni, Mhe. Rais aliahidi kujenga barabara ya kilometa tatu katika Mji wa Kakonko ambao ndiyo Makao Makuu ya Wilaya.

Je, kwa nini ahadi hiyo haijatekelezwa na ni lini sasa itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Jimbo la Buyungu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza kutekeleza ahadi ya aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa awamu. Katika mwaka wa fedha 2020, Serikali imeanza ujenzi wa barabara yenye urefu wa mita 630 kwa kiwango cha lami katika Mji wa Kakonko itakayogharimu shilingi milioni 500. Ujenzi huu umefikia asilimia 80 na unatarajiwa kukamilika mwezi Mei 2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya barababara nchini ikiwemo Wilaya ya Kakonko kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. ALOYCE A. KWEZI - K.n.y. MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-


Je, Serikali imechukua hatua gani kukabiliana na upungufu wa walimu na madawati hasa baada ya elimu ya msingi na sekondari kuwa bure?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE.DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuajiri walimu wa shule za msingi na sekondari ambapo kuanzia mwaka fedha 2016/2017 hadi 2020/2021 walimu 33,684 na mafundi sanifu maabara 497 wameajiriwa. Aidha, Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia itaajiri walimu 6,000 ifikapo tarehe 30 Julai, 2021 ikiwa ni utekelezaji wa ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukabiliana na upungufu wa madawati katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi bilioni 7.15 kwa ajili ya kutengeneza madawati 710,000 katika shule za msingi. Aidha, Serikali inaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo pamoja na wananchi katika kutatua changamoto ya madawati kwenye Shule za Msingi na Sekondari nchini.
MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:-

Utaratibu wa watoto kuingia darasa la kwanza ni lazima awe amepitia shule za awali.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuimarisha madarasa ya elimu ya awali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, elimu ya awali ni muhimu katika kumwandaa na kumjengea msingi mwanafunzi wakati wote atakapokuwa anaendelea na masomo katika ngazi zote. Kwa kuzingatia suala hili, Serikali ilitoa maagizo kuwa kila shule ya msingi nchini iwe na darasa la awali ili kuwapokea wanafunzi walio na umri kati ya miaka minne hadi mitano ikiwa ni maandalizi ya kujiunga na darasa la kwanza.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanda Mtaala wa Elimu ya Awali unaoendana na aina ya ujifunzaji unaotakiwa kwa watoto wa elimu ya awali. Mtaala huo umezingatia ujifunzaji kwa kutumia michezo. Hadi Februari 2021, walimu 70,712 wanaofundisha darasa la awali, la Kwanza na la Pili wamepatiwa mafunzo ya namna ya utumiaji wa mbinu sahihi za ufundishaji, ufaraguzi na utumiaji wa zana za kufundishia. Hatua hii imeimarisha ufundishaji na ujifunzaji katika madarasa ya awali nchini.

Mheshimiwa, Serikali imezielekeza Halmashauri zote nchini kuhakikisha kuwa watoto wa Darasa la Awali, la Kwanza na la Pili wanapatiwa vyumba vya bora vya madarasa vinavyowawezesha kutengeneza mazingira bora ya kujifunzia kwa rika lao na kuhakikisha kuwa mtoto wa Darasa la Awali analindwa na kupata eneo zuri la kujifunzia kwa kucheza ndani na nje ya darasa. Hatua hii pia imehusisha kubadilisha madarasa haya kwa kuweka zana za ujifunzaji.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuboresha miundombinu na kuwajengea uwezo walimu wanaofundisha Elimu ya Awali katika shule zote nchini kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

MHE. HASSAN S. MTENGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara za lami katika Kata za Ufukoni, Magomeni na shangani Manispaa ya Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais–TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Selemani Mtenga Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kujenga mundombinu ya barabara nakufanya matengenezo katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018 kupitia Miradi ya Uendelezaji Miji yaani Tanzania Strategic Cities Projects Serikali ili jenga barabara za lami zenye urefu wa kilomita 4.53 katika Kata ya Shangani Manispaa Mtwara Mikindani kwa gharama ya shilingi bilioni 7.09. Aidha, katika mwaka wa fedha 2019/ 2020 kupitiafedha za Mfuko wa Barabara Serikali imejenga barabara za lami zenye urefu wa kilomita 0.85 katika Kata ya Shangani kwa gharama ya shilingi milioni 232.98. Vilevile, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 117.38 kwa ajili ya ujenzi wa barabara za lami zenye urefu wa kilomita 0.55 kwa kiwango cha lami katika mtaa wa Maduka Makubwa ambapo mkandarasi anaendelea na ujenzi.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/21 barabara zenye urefu wa kilomita 22.37 zimefanyiwa matengenezo na kilomita 1.3 zinaendelea na matengenezo kwa gharama ya shilingi milioni 74.19 katika Kata za Ufukoni na Magomeni. Serikali inatambua ukuaji wa haraka wa Mji wa Mtwara naitaendelea kuupa kipaumbele cha barabara za lami na mifereji ya maji ya mvua kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuipa fedha Halmashauri ya Temeke ili iweze kujenga Shule mpya za kutosha kutokana na Jimbo la Mbagala kuongoza kuwa na wanafunzi wengi wa Shule za Msingi na Sekondari?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Abdallah Chaurembo, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha miundombinu ya elimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke, katika mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2019/2020 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Temeke Shilingi milioni 724 kwa ajili ya ujenzi wa Shule mpya ya Msingi ya Marten Lumbanga na Shule ya Msingi Dovya. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/ 2021 Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kupitia mapato yake ya ndani imejenga jengo la ghorofa moja kwa ajili ya Kidato cha Tano na Sita katika Shule ya Sekondari Mbagala kwa gharama ya shilingi bilioni 1.056.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imeitengea Halmashauri ya Wilaya ya Temeke shilingi bilioni 1.74 ambapo shilingi bilioni 1.53 zitaelekezwa katika Jimbo la Mbagala kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya katika Kata ya Chamazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali ilikamilisha maboma 10 ya madarasa ya Shule za Msingi katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kwa gharama ya Shilingi milioni 137.5. Aidha, kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2019/2020 Serikali imejenga madarasa mapya 25 ya Shule za Msingi katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kwa gharama ya shilingi milioni 500.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2020/ 2021 Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kupitia mapato yake ya ndani imejenga vyumba 76 vya madarasa ya Shule za Sekondari kwa gharama ya shilingi bilioni 1.72. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga Shilingi milioni 220 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba 11 vya madarasa ya Shule za Sekondari katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke. Vilevile, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Shilingi milioni 209 zimetengwa kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya Shule za Sekondari.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA - K.n.y. MHE. SALIM A. HASHAM aliuliza:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani kutengeneza barabara za Ulanga na kutenga bajeti ya dharura ili TARURA iweze kukarabati barabara mara tu zinapoharibika?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuipatia TARURA ya Halmashauri Ulanga usafiri ili kuongeza ufanisi katika kazi zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Alaudin Hasham Salim, Mbunge wa Jimbo la Ulanga, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha miundombinu ya barabara katika Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga, Serikali imeongeza fedha za matengenezo ya barabara kutoka shilingi milioni 471.49 katika mwaka wa fedha 2020/2021 hadi shilingi 671.49 katika mwaka wa fedha 2021/2022 ikiwa ni ongezeko la asilimia 42.4. Aidha, Serikali imekuwa ikitenga 5% ya bajeti ya fedha za matengenezo ya barabara kwa ajili ya kazi za dharura. Kupitia fedha za dharura, TARURA katika Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga imejenga madaraja ya Epanko na Ikangao kwa gharama ya Shilingi milioni 64.5 katika mwaka wa fedha 2018/2019.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua mahitaji ya magari kwa ajili ya usimamizi wa miradi ya barabara na uendeshaji wa ofisi za Mameneja wa TARURA katika Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga. Wakala una magari 192 yaliyopo katika hali nzuri kwenye Mikoa na Halmashauri, magari 107 mabovu na magari 15 katika Ofisi za Makao Makuu.

Katika mwaka wa fedha 2020/2021 TARURA imetenga shilingi bilioni 2.8 kwa ajili ya ununuzi wa magari 26 na pikipiki tisa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 TARURA imeidhinishiwa shilingi bilioni 2.8 kwa ajili ya ununuzi wa magari 30. Magari hayo yatapelekwa kwenye Halmashauri mbalimbali ambazo hazina magari na Halmashauri ambazo hazina Magari kama Ulanga, zitapewa kipaumbele. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza:-

Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami katika Mji wa Mbinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas William Mbunda, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mbinga Mji, ina barabara zenye urefu wa kilomita 7.45 zilizojengwa kwa kiwango cha lami zikiwemo kilomita 0.2 zilizojengwa katika mwaka wa fedha 2020/2021 kwa gharama ya shilingi milioni 170. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa barabara ya Mbuyula Hospitali hadi Ikulu ndogo yenye urefu wa kilomita moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya barabara nchini kote ikiwemo Halmashauri ya Mji wa Mbinga kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. FELISTA D. NJAU aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukamilisha ujenzi wa barabara ya Kairuki hadi Mikocheni Shoppers ambayo hadi sasa imejengwa kipande kidogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Felista Deogratias Njau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Kairuki hadi Mikocheni Shoppers inayojulikana kwa jina la Barabara ya Warioba - Chakwu yenye urefu wa kilomita 1.73 ilijengwa kwa kiwango cha lami kipande cha kilometa 1.13 kwa gharama ya shilingi bilioni 1.017 katika mwaka wa fedha 2014/2015. Hivyo, kipande chenye urefu wa kilomita 0.6 hakikujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii yote inahitaji matengenezo makubwa kikiwemo kipande cha kilometa 0.6 ambacho hakina lami. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 TARURA Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni imepanga kufanya tathmini ya barabara hii na Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kujenga na kuifanyia matengenezo barabara hii kwa mujibu wa matokeo ya tathmini.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Makanya kwenda kwenye Machimbo ya Jasi Wilayani Same?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena Athumani Bushiri, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Makanya hadi kwenye Machimbo ya Jasi Wilayani Same ina urefu wa kilometa 40.9. Kipande cha kilometa 4.5 cha barabara hii kimeinuliwa kwa kujengwa tuta kati ya kilometa 14.5 zinazotakiwa kujengewa tuta kwa kiwango cha changarawe. Kipaumbele cha Serikali ni kuhakikisha kuwa barabara hii inapitika muda wote na ndiyo maana imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya matengenezo ya mara kwa mara.

Katika mwaka wa fedha 20219/2020, Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Same umefanya matengenezo ya barabara ya Makanya hadi kwenye Machimbo ya Jasi maeneo korofi yenye urefu wa kilometa 3.54 kwa gharama ya shilingi milioni 77.36.

Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021, TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Same imefanya matengenezo ya barabara hiyo kipande chenye urefu wa kilometa mbili kwa kiwango cha changarawe kwa gharama ya shilingi milioni 49.4. Vilevile katika mwaka wa fedha 2021/2022 jumla ya shilingi milioni 61.25 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha changarawe yenye urefu wa kilomita moja pamoja na ujenzi wa makalavati 14.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa barabara ya Makanya hadi kwenye Machimbo ya Jasi na itaendelea kuifanyia matengenezo ili kuhakikisha inapitika. Serikali itatoa kipaumbele cha ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami katika bajeti zijazo ili kuiboresha na kurahisisha usafirishaji wa Jasi.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:-

Je, ni lini barabara za kutoka Rubanga – Isulwabutundwe – Mkoba -Kukuruma – Kamhanga - Kishinda na Mkolani zitatengewa fedha na TARURA kwa ajili ya ujenzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Musukuma Joseph Kasheku, Mbunge wa Geita Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vilivyotajwa vinaunganishwa na barabara za Mkoba Bridge – Isulwabutundwe – Lubanga yenye urefu wa kilometa 15 na Geita – Isamilo – Mkolani kwa maana ya Busekeseke yenye urefu wa kilometa 18 ni barabara muhimu sana kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mpango wa utekelezaji kwa mwaka wa fedha 2020/2021 barabara hizi zimetengewa jumla ya fedha shilingi milioni 318.83 kwa ajili ya matengenezo ya kilometa 33 na wakandarasi wanaendelea na utekelezaji wa kazi. Kazi zinatarajiwa kukamilishwa mwezi Julai mwaka, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini itaendelea kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kuzifanyia matengenezo barabara zote zilizopo Wilaya ya Geita Vijijini kwa kulingana na upatikanji wa fedha.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali italipatia Jimbo la Busanda Vituo vya Afya hususan Tarafa ya Butundu na Tarafa ya Busanda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tumaini Bryceson Magessa, Mbunge wa Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Busanda katika Wilaya ya Geita lina Vituo vya Afya vitano ambapo vituo vya Afya vitatu vya Nyarugusu, Kashishi na Bukoli vipo katika Tarafa ya Busanda na Vituo vya Afya viwili vya Chikobe na Katoro vipo katika Tarafa ya Butundwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuendelea kuboresha huduma za afya katika Wilaya ya Geita kuanzia mwaka wa fedha 2018/2019 hadi 2019/2020 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Geita shilingi bilioni 2.8 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Geita; shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Katoro na shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Nyarugusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu na shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali ya Wilaya ya Geita. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi bilioni 1.9 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Geita na Hospitali ya Katoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Halmashauri ya Wilaya ya Geita imetengewa shilingi milioni 200 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma manne ya zahanati, yakiwemo maboma ya Zahanati za Lubanda na Bujura katika Jimbo la Busanda. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri ya Wilaya ya Geita imetengewa fedha shilingi milioni 375 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Kituo cha Afya Isulwabutundwe na shilingi milioni 375 kwa ajili kuanza ujenzi wa Kituo cha Afya Butobela.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya huduma za afya katika Jimbo la Busanda, ikiwemo kujenga zahanati, vituo vya afya na hospitali kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaunga mkono juhudi za wananchi katika ujenzi wa Zahanati na Vituo vya Afya Kata za Arumeru Mashariki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuunga mkono jitihada za wananchi katika Halmashauri zote nchini kwa kutoa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya miundombinu ya afya kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Meru shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati za Ngabobo, Shishtoni na Mikungani.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati za Ngejisosia, Imbaseni na Msitu wa Mbogo. Vilevile katika mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri kupitia mapato yake ya ndani imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Maroroni.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kushirikiana na wananchi kuboresha miundombinu ya afya ikiwemo maboma ya zahanati na vituo vya afya kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA (K.n.y. MHE. CATHERINE V. MAGIGE) aliuliza:-

Je, Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka wa kuongeza bajeti ya TARURA Wilayani Ngorongoro ili kukabiliana na uharibifu wa barabara uliotokana na mvua kubwa zilizonyesha msimu wa mwaka 2019 na 2020?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Valentine Magige, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na changamoto ya uharibifu wa miundombinu ya barabara inayotokana na mvua kubwa zilizonyesha msimu wa mwaka 2019 na 2020, Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro katika mwaka wa fedha 2019/2020, ulifanya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 94.4, vivuko 15 na daraja moja kwa gharama ya shilingi bilioni 1.08. Aidha, hadi kufikia Aprili, 2021, Serikali imeipatia TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro shilingi milioni 917.64 kati ya shilingi bilioni 1.05 zilizotengwa katika mwaka wa fedha 2020/2021 kwa ajili ya matengenezo ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020 sambamba na matengenezo ya kawaida, Serikali iliipatia TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro shilingi milioni 276.68 kwa ajili ya matengenezo ya dharura katika barabara zilizoharibiwa na mvua. Barabara zilizotengenezwa ni pamoja na kipande chenye urefu wa kilomita 1.2 na makalavati manne katika barabara ya Oldonyowas - Ormania mpaka Pipaya, ujenzi wa makalavati manne na madrifti matano katika barabara ya Mdito – Digodigo – Oldonyosambu na matengenezo ya kipande chenye urefu wa kilomita 1.5 na drifti moja katika barabara za Ormania mpaka Oldonyorock.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 shilingi bilioni 1.04 zimetengwa kwa ajili ya matengenenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 105, mifereji yenye urefu wa kilomita 1.1 na makalavati 30. Serikali itaendelea kuongeza fedha zinazotengwa kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. DAVID M. KIHENZILE K.n.y. MHE. NANCY H. NYALUSI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi na kuanza kutumia Hospitali ya Wilaya ya Mufindi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nancy Hassan Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu katika Hospitali ya Halmashauri. Hadi Aprili 2021, ujenzi wa majengo saba ambayo ni jengo la utawala, jengo la huduma kwa wagonjwa wa nje kwa maana ya OPD, jengo la maabara, jengo la mionzi, jengo la wazazi, jengo la kuhifadhia dawa, jengo la kufulia umekamilika na ujenzi wa wodi ya watoto na wodi ya magonjwa mchanganyiko kwa wanaume na wanawake upo katika hatua ya upandishaji wa ukuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya ya Mufindi. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la upasuaji, jengo la kuhifadhia maiti na wodi ya upasuaji kwa wanaume na wanawake. Hospitali ya Wilaya ya Mufindi imeanza kutoa huduma za wagonjwa wa nje na inatarajiwa ifikapo mwishoni mwa mwaka 2022 hospitali hiyo itaanza kutoa huduma kwa zaidi ya asilimia 90 ya huduma zote zinazotakiwa kutolewa katika ngazi ya Hospitali ya Halmashauri.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-

Je, ni lini barabara ya Kiloba – Njugilo yenye urefu wa kilometa 7 itajengwa ili kurahisisha mawasiliano ya wananchi na wanafunzi wanaokwenda Kata ya Masukulu – Rungwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge Viti Maalum, kama Ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Kiloba-Njugilo ni barabara inayounganisha Kata mbili za Bujela na Masukulu. Kwa kutambua umuhimu wake, barabara ya Kiloba-Njugilo ipo kwenye hatua za uhakiki ili iweze kuingizwa kwenye Mfumo wa Barabara za Wilaya kwa maana ya DROMAS ili iweze kupatiwa fedha za Mfuko wa Barabara kwa ajili ya matengenezo na ujenzi. Utaratibu wa kuingizwa kwenye mfumo wa barabara za Wilaya ukikamilika barabara hiyo itatengewa fedha kupitia fedha za Mfuko wa Barabara kwa maana ya Road Fund ili iweze kujengwa walau kwa kiwango cha changarawe na kuiwezesha kupitika katika majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imejenga Daraja la Kigange linalounganisha Vijiji vya Kiloba na Mwalisi kwa gharama ya shilingi milioni 46.8.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE K.n.y. MHE. ABEID R. IGHONDO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara za Singida Kaskazini zinazounganisha Vijiji ambazo hazipitiki kwa sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aysharose Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Singida Kaskazini ina mtandao wa barabara wenye urefu wa kilometa 811.68 ambao umekuwa ukifanyiwa matengenezo pamoja na kujenga na kukarabati vivuko. Katika mwaka wa fedha 2019/2020, TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Singida ilifanya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 78.55 na vivuko 22 kwa gharama ya shilingi milioni 739.39.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka fedha 2020/2021, barabara zenye urefu wa kilometa 67.8 na vivuko 20 vimetengenezwa kwa gharama ya shilingi millioni 711.08 ambapo hadi Machi, 2021 barabara zenye urefu wa kilomita 45 na vivuko 15 vimekamilika. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 barabara zenye urefu wa kilomita 62.5 na vivuko 24 vitajengwa kwa gharama ya shilingi millioni 711.08.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini Halmashauri ya Wilaya ya Singida itafanya tathmini ya barabara zote za Singida Kaskazini ili kuandaa mpango wa namna bora ya kuweka vipaumbele vya ujenzi na matengenezo ya barabara.
MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:-

Je, ni lini serikali itakuwa tayari kuanza mradi wa TACTIC ili kufikia Malengo Makuu ya Serikali ya mwaka 2020 – 2025 katika kuboresha miundombinu ya barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Shing’oma Mabula, Mbunge wa Jimbo la Nyamagana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Uendelezaji Miundombinu katika Miji (TACTIC) unatarajiwa kutekelezwa katika Halmashauri za Miji 45 nchini. Mradi unatarajiwa kutekelezwa na Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa fedha za mkopo wenye masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia. Serikali inaendelea na mazungumzo na Benki ya Dunia kuhusu upatikanaji wa fedha hizo na mradi utaanza kutekelezwa baada ya kukamilika kwa majadiliano na fedha kutolewa.
MHE. FRANCIS I. MTINGA aliuliza:-

Je ni lini Serikali itaweka vifaa vya maabara kwenye maabara zote za Shule za Sekondari katika Wilaya ya Mkalama zilizojengwa kwa nguvu za wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Iramba Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama ina jumla ya shule 20 za Sekondari ambapo 19 kati ya hizo ni shule za Serikali. Usambazaji wa vifaa vya maabara mashuleni huzingatia ukamilishaji wa vyumba vya maabara katika shule husika. Hadi Machi, 2021, Serikali imepeleka vifaa vya maabara kwenye shule 18 kati ya shule 19 za sekondari katika Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, shule ya sekondari Kikhonda haijapelekewa vifaa kwa sababu haina vyumba vya maabara. Hata hivyo, Halmashauri kwa kushirikiana na wananchi wa Kata ya Kikhonda wameanza taratibu za ujenzi wa maabara katika shule hiyo ili ujenzi utakapokamilika iweze kuingizwa kwenye mpango wa kupatiwa vifaa.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza:-

Je, ni sheria ipi ambayo ilitumika kuchukua ardhi ya Mlima Nkongore kutoka kwa wananchi na kulipatia Jeshi la Magereza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi. Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Kembaki Michael, Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mlima Nkongore upo katika Halmashauri ya Mji Tarime na una eneo lenye ukubwa wa ekari 266.65. Eneo hilo halina mchoro wa mipango miji na halijamilikishwa. Wananchi wanaozunguka eneo hilo walikuwa wakiutumia Mlima Nkongore kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo ukataji kuni, uchomaji mkaa na kilimo, shughuli ambazo zilikuwa zinahatarisha mazingira ya Mlima Nkongore.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi Novemba, 2017 Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Tarime ilikabidhi eneo hilo kwa Jeshi la Magereza ili kuhakikisha kuwa eneo hilo linalindwa kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira Na. 20 ya mwaka 2004 kwa maana ya Environmental Management Act, 2004; kifungu cha 58(1) na (2) ambacho kinazuia kufanya shughuli zozote zinazoweza kusababisha hifadhi ya mlima kuharibiwa. Halmashauri ya Mji Tarime kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira inakamilisha taratibu za kulifanya eneo la Mlima Nkongore kuwa hifadhi. Hivyo, eneo la Mlima Nkongore litaendelea kuwa chini ya uangalizi wa Magereza hadi hapo taratibu zitakapokamilika na kulitangaza kuwa eneo hilo kuwa hifadhi.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA - K.n.y. MHE. MICHAEL C. MWAKAMO aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua migogoro ya mipaka ya kiutawala baina ya Mikoa, Wilaya na Vijiji hapa nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Michael Constantino Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua migogoro ya mipaka ya kiutawala baina ya Mikoa, Wilaya na Vijiji hapa nchini Serikali imechukua hatua mbalimbali ikiwemo kusambaza Matangazo ya Serikali kwa maana ya Government Notices au GN yanayoonesha mipaka ya Wilaya na Mikoa kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya zote nchini; kKuunda vikundi kazi na kuvipeleka kwenye maeneo yenye migogoro ya mipaka ili kutatua migogoro; kusimamia utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Matumizi Bora ya Ardhi nchini kwa kuhakikisha Vijiji, Kata na Wilaya zinaandaa na kutekeleza Mipango ya matumizi ya ardhi, kutoa elimu kwa umma kuhusu Sera na Sheria za ardhi, kusimamia upimaji wa viwanja na mashamba katika Halmashauri, kurasimisha makazi na kumilikisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ili kutatua migogoro ya mipaka ya kiutawala baina ya Mikoa, Wilaya na Vijiji hapa nchini.
MHE. ESTER A. BULAYA K.n.y. MHE. CHARLES M. KAJEGE aliuliza:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuipunguzia mzigo TARURA kwa kuzihamishia TANROADS barabara za Bulamba – Karukekere – Nakatubai – Igunchi – Mwitende na Busambara - Mugara zilizopo katika Jimbo la Mwibara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Charles Mugeta Kajege, Mbunge wa Jimbo la Mwibara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mapendekezo ya kupandisha hadhi barabara kutoka barabara za Wilaya na kwenda barabara za Mikoa yanatakiwa kuwasilishwa na kujadiliwa kwenye Vikao vya Bodi ya Barabara ya Mkoa. Endapo Bodi itaridhia mapendekezo hayo, yanatakiwa kuwasilishwa kwa Waziri mwenye Dhamana na barabara ambaye ni Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, hatua inayofuata ni maombi hayo kupitiwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi chini ya Kamati ya Kitaifa ya Kupandisha Hadhi Barabara ili kuona kama yanakidhi vigezo na Kamati kuridhia au kukataa kupandishwa hadhi barabara husika. Hivyo, nashauri utaratibu huo ufuatwe katika maombi ya kupandisha hadhi barabara za Bulamba – Karukekere - Nakatubai – Igunchi - Mwitende na Busambara - Mugara zilizo katika Jimbo la Mwibara.
MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza: -

Je, lini Serikali itaanza kujenga Barabara ya Kijiji cha Uzena kwenda Kijiji cha Njomlole katika Jimbo la Mbinga Mjini kwa kiwango cha changarawe ili iweze kupitika kwa wakati wote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas William Mbunda, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara inayounganisha Vijiji vya Uzena na Njomlole inayojulikana kama barabara ya Masimeli – Njomlole na ina urefu wa kilomita 5.5, katika mwaka wa fedha 2021/2022 TARURA, Halmashauri ya Mji Mbinga imetenga Shilingi milioni 10 kwa ajili ya matengenezo ya barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022, Wakala wa Barabara za Vijijni na Mijini umepanga kufanya tathmini ya miundombinu ya barabara na madaraja nchini kote ikiwemo Jimbo la Mbinga Mjini ili kuandaa mpango wa namna bora ya kutoa kipaumbele cha ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara na madaraja.
MHE. MOHAMED L. MONNI aliuliza:-

Je, ni lini Barabara ya Kwamtoro – Sanzawa – Mpendo yenye kilomita 58.2 itajengwa kwa kiwango cha kupitika msimu mzima kwani kwa sasa imekatika kutokana na mvua kubwa na kutojengwa kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/ 2021, TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Chemba imetenga shilingi milioni 84.04 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Kwamtoro – Sanzawa – Mpendo yenye urefu wa kilomita 23. Ujenzi wa barabara hii unaendelea ambapo matengenezo ya barabara yenye urefu wa kilomita 10, makalvati mawili na drift moja umekamilika. Katika mwaka wa fedha 2021/2022, jumla ya shilingi milioni 42 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara yenye urefu wa kilomita 10 na ujenzi wa makalavati matatu.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 pamoja na kazi nyingine Wakala wa barabara za Vijijini na Mijini, umepanga kufanya tathmini ya miundombinu ya barabara zake zote ikiwemo za Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ili kuandaa mpango wa namna bora ya kutoa vipaumbele vya ujenzi na matengenezo ya barabara na madaraja. Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara ikiwemo ya barabara ya Kwamtoro – Sanzawa –Mpendo kwa kadri ya upatikanaji wa fedha ili kuimarisha usafiri na usafirishaji.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara tatu za Lukoma – Lubalisi, Kalya – Ubanda na Kalya – Sibwesa zinazounganisha Mkoa wa Kigoma kupitia Wilaya ya Uvinza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, asante sana; kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020 barabara za Lukoma - Lubalisi, Kalya - Ubanda na Kalya - Sibwesa zilitambuliwa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) na kuwekwa kwenye mfumo wa barabara zinazotambuliwa na TARURA (DROMAS). Barabara hizo zitaingizwa kwenye mpango wa matengenezo ya barabara kupitia fedha za matengenezo ya barabara zinazotolewa kwa TARURA katika kila Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Wananchi pamoja na Shirika la Maendeleo la Ubelgiji la Kuendeleza Kilimo – Kigoma (SAKIRP) inaendelea na ujenzi wa madaraja 10 kwa kutumia teknolojia ya mawe kwa gharama ya shilingi milioni 190 ambapo madaraja matatu yamekamilika likiwemo Daraja la Mto Ruega katika barabara ya Kalya – Ubanda lililojengwa kwa shilingi milioni 37 katika mwaka wa fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha katika bajeti zake ili kuzifanyia matengenezo barabara hizo kwa kadiri upatikanaji wa fedha utakavyoendelea kuimarika.
MHE. CECIL D. MWAMBE K.n.y. MHE. MWANTUM M. ZODO aliuliza:-

Kada ya Elimu inakadiriwa kuwa na upungufu wa walimu takribani 60,000.

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kukabiliana na changamoto hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA - (MHE. DAVID E. SILINDE): alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantum Mzamili Zodo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Serikali ni kuendelea kuajiri na kujaza nafasi zilizoachwa wazi kwa walimu waliokoma utumishi wao kwa sababu mbalimbali kama vile kufariki, kustaafu na walioachishwa kazi kwa mashauri mbalimbali ya kinidhamu. Aidha, Mwezi Mei 2021 Ofisi ya Rais- TAMISEMI imetangaza ajira 6,949 za walimu wa shule za msingi na sekondari ili kukabiliana na changamoto ya uhaba wa walimu.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuajiri walimu wa shule za msingi na sekondari nchini kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa maboma ya Shule za Sekondari Bombo na Ndungu ili Kidato cha Tano kianze baada ya mabweni ya wasichana kukamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Shule za Sekondari Bombo na Ndungu zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Same ni shule za kutwa zinazopokea wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne. Serikali ina mpango wa kuzipandisha hadhi shule hizi ili ziweze kuchukua wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita. Katika kutekeleza mpango huo katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Same shilingi milioni 150 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni mawili katika Shule ya Sekondari Bombo na shilingi milioni 75 kwa ajili ya ujenzi wa bweni moja katika Shule ya Sekondari Ndungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa bweni moja katika Shule ya Sekondari Bombo umekamilika na ujenzi wa bweni moja unaendelea; na ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari Ndungu umekamilika. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Same shilingi milioni 50 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari Bombo na shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa bwalo la chakula katika Shule ya Sekondari Ndungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Same kwa kushirikiana na wananchi inaendelea na ujenzi wa vyumba vinne vya madarasa katika Shule ya Sekondari Ndungu. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 120 kwa ajili ya ujenzi wa bweni moja na maktaba ya TEHAMA katika Shule ya Sekondari Ndungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi Septemba, mwaka 2022 hivyo kuwezesha Shule hizo kuanza kuchukua wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea TARURA fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara kwa kuzingatia ukuaji wa kasi wa Miji na Halmashauri zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Jonathan Msambatavangu, Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2021/ 2022, Serikali imeitengea TARURA shilingi bilioni 400 kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara na madaraja. Bajeti hiyo ni ongezeko la shilingi bilioni 124.97 kutoka bajeti ya shilingi bilioni 275.03 iliyotengwa kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara na madaraja katika Mwaka wa Fedha 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, sambamba na kuipatia TARURA fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara na madaraja, Serikali imeendelea na ujenzi wa miundombinu katika miji inayokua kupitia mipango mbalimbali kama vile Mpango wa Uboreshaji wa Miji Mikakati ambayo ilihusisha Majiji na Manispaa kupitia Mradi wa Uendelezaji Miji ya Kimkakati (TSCP), Programu ya Kuimarisha Halmashauri za Miji 18 (ULGSP) ikiwemo Halmashauri ya Manispaa ya Iringa na Mradi wa Uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam (DMDP).

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na maandalizi ya Mradi wa Kuboresha Miundombinu ya Mijini (TACTIC) na Mradi wa Uendelezaji wa Miundombinu ya Mkoa wa Dar es Salaam, awamu ya pili (DMDP II) kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ikiwemo barabara, madaraja, stendi za mabasi na masoko.
MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:-

Je, kwa nini wazazi wanachangishwa michango ya kuchangia elimu wakati Serikali inasema Elimu kwa Shule ya Msingi na Sekondari ni bure?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Waraka wa Elimu Na.5 wa mwaka 2015 iliamua kutoa elimumsingi bila malipo kuanzia elimu ya awali hadi kidato cha nne. Uamuzi huo ulijielekeza katika kutekeleza Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 ambayo ina lengo la kuhakikisha watoto wote wa Kitanzania wenye rika la elimumsingi wanapata elimu bila kikwazo chochote ikiwemo ada au michango. Aidha, Serikali ilitoa Waraka wa Elimu Na.3 wa mwaka 2016 kuhusu utekelezaji wa elimumsingi bila malipo. Waraka huu unafafanua maana ya elimumsingi na kuainisha majukumu ya kila kundi linalohusika katika utoaji wa elimumsingi bila malipo na kuweka utaratibu wa utekelezaji wake.

Mheshimiwa Spika, majukumu ya jamii na wananchi kuhusu michango yamebainishwa kwenye Waraka wa Elimu Na.3 wa mwaka 2016. Waraka unaeleza kuwa Kamati za Shule au Bodi za Shule zitashirikisha jamii katika maazimio na maamuzi ya masuala mbalimbali yanayohusu maslahi na maendeleo ya shule hususan uchangiaji wa hiari na kuwasilisha maamuzi hayo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ili kupata kibali. Hivyo, uchangiaji katika elimu unaoruhusiwa ni wa hiari na hauhusishi wanafunzi kuzuiwa kuhudhuria masomo.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA K.n.y. MHE. CATHERINE V. MAGIGE aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kubadili Shule za Msingi za Tarafa ya Ngorongoro kuwa bweni ilikunusuru maisha ya wanafunzi ambao wamekuwa wakitembea umbali mrefu na kuhatarisha maisha yao kutokana na wanyamapori kwani eneo kubwa la Tarafa hiyo ni sehemu ya hifadhi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Valentine Magige, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa Shule za Msingi za Tarafa ya Ngorongoro kuwa za bweni. Serikali kwa kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali wa elimu imeanzisha shule tatu za bweni ambazo ni Nainokanoka, Enduleni na Olbalbal zenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 1,014 wakiwemo wavulana 590 na wasichana 424. Shule hizo zinachukua wanafunzi wanaotoka maeneo ambayo yana wanyama wakali na yaliyo mbali na maeneo ya shule na hivyo kuwawezesha wanafunzi kuhudhuria masomo bila vikwazo vyovyote.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuongeza mabweni katika shule hizo ili kuziwezesha kuchukua wanafunzi wengi zaidi.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza:-

Je lini Serikali itaajiri walimu wa masomo ya sayansi katika Shule za Sekondari za Halmashauri ya Mji Mbulu ili wanafunzi wapate ujuzi wa masuala ya sayansi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paul Issaay , Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2016/2017 hadi 2019/2020 Serikali imeajiri na kuwapanga walimu 17 wa sayansi na hisabati na mafundi sanifu wa maabara wawili katika Halmashauri ya Mji Mbulu kati ya walimu 10,418 wa Sekondari na mafundi sanifu maabara 397 walioajriwa katika kipindi hicho.

Aidha, Serikali inaendelea kuratibu zoezi la kuajiri walimu 6,949 kwa nafasi za ajira zilizotangazwa mwezi Mei, 2021 ambao watapangwa kwenye shule mbalimbali zikiwemo na shule za Halmashauri ya Mji Mbulu.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI K.n.y. MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kutekeleza ahadi iliyotolewa na Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa Barabara ya Bomang’ombe – Rudugai – Chekimaji – Kikafu chini – Kawaya – Mijengweni – Shing’oro Mferejini hadi Makoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Bomang’ombe – Rudugai – Chekimaji – Kikafu Chini – Kawaya – Mijengweni hadi Shing’oro Mferejini hadi Makao zimesajiliwa kwa majina ya Bomang’ombe – Kikafu Chini na ina urefu wa kilomita 26.53.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Shing’oro – Mijengweni hadi Makoa yenye urefu wa kilomita 12.7 na Barabara ya Mferejini – Makoa yenye urefu wa kilomita 21 ni barabara muhimu katika Halmashauri ya Hai na zinahudumiwa na Wakala wa Barabara Vijijini wa Wilaya ya Hai. Serikali inatambua kuwa barabara hizi ni miongoni mwa barabara zilizoahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami katika ahadi za Rais na Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kutekeleza ahadi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuzifanyia matengenezo barabara hizo ili kuhakikisha zinapitika katika majira yote ya mwaka. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, TARURA Halmashauri ya Hai iliidhinishiwa shilingi milioni 72 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Bomang’ombe – Kikafu Chini kipande chenye urefu wa kilomita 14 kwa shilingi milioni 35 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Shing’oro – Mijengweni kipande chenye urefu wa kilomita 4 na sShilingi milioni 67.5 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Mferejini – Makoa kipande chenye urefu wa kilomita 6.4 ambapo matengenezo ya barabara hizo yanaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, TARURA Halmashauri ya Hai imetengewa jumla ya shilingi milioni 628.2 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Bomang’ombe – Kikafu Chini kipande chenye urefu wa kilomita 10 na boksi kalvati moja la Shing’oro – Mijengweni kipande chenye urefu wa kilomita 8 na ujenzi wa barabara ya Mferejini – Makoa kwa kiwango cha changarawe kwa kilomita 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi na kutekeleza ahadi za Rais za ujenzi wa barabara za lami katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Halmashauri ya Hai.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza:-

Je, ni lini ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa barabara ya lami yenye urefu wa Kilomita tano ndani ya Mji wa Bagamoyo itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Muharami Shabani Mkenge, Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutekeleza ahadi ya Rais ya ujenzi wa barabara za lami zenye urefu wa kilomita 5 iliyotolewa katika mwaka wa fedha 2015 ambapo hadi mwaka 2019/2020 barabara zenye urefu wa kilomita 2.36 zimejengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 2.37. Barabara hizo zinajumuisha Barabara ya Stendi ya Kongowe – Kwa Chambo kilomita 0.6, Mgonera – Forodhani kilomita 0.63, Rubeya kilomita 0.7 na Soko la Uhindini kilomita 0.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha wa 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 375 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Bomani kipande chenye urefu wa kilomita 0.4 kwa kiwango cha lami. Tayari Mkandarasi ameshapatikana na yupo kwenye maandalizi ya kuanza kazi. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 375 kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Kapala kwa kiwango cha lami yenye urefu wa kilomita 0.45.
MHE. NICODEMUS H. MAGANGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara zote mbovu zilizopo katika Jimbo la Mbogwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemus Henry Maganga, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mbogwe lipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe lina mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 1,344.3. Serikali imekuwa ikifanyia matengenezo ya barabara mbovu, pamoja na matengenezo ya kawaida kwa barabara zenye hali nzuri kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika mwaka wa fedha 2019/2020, Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe iliidhinishiwa shilingi bilioni 1.30 kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 78.6, makalvati mistari 27, boksi kalvati moja pamoja na ujenzi wa barabara ya Mang’ombe – Magetini mpaka Kona nne, yenye urefu wa kilometa 1.2. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, jumla ya shilingi bilioni 1.64 ziliidhinishwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 46.6, makalvati mistari 18 pamoja na ujenzi wa barabara ya Masumbwe – Iponya yenye urefu wa kilometa moja kwa kiwango cha lami na barabara ya Mang’ombe, Magetini – Kona nne, yenye urefu wa kilomita 0.8 kwa kiwango cha lami, ujenzi wa barabara hizo umekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, Katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi bilioni 1.14 kwa ajili ya matengenezo ya barabara yenye urefu wa kilometa 74.96, Mtaro wa mawe kilometa 1.2 na ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa moja kwa kiwango cha lami katika Mji wa Masumbwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matengenezo yaliyofanyika katika mwaka wa fedha 2019/2020 na 2020/2021, yamejumuisha barabara muhimu zilizokuwa mbovu katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe, zikiwemo barabara ya Shenda - Mwabomba yenye urefu wa kilometa 17, barabara ya Isebya-Lwamgas yenye urefu wa kilometa 10. Barabara ya Ushirika-Kadoke-Ntono yenye urefu wa kilomita 5.5, barabara ya Ikunguigazi – Isabya - Nyashinge yenye urefu wa kilometa 15, barabara ya kanegere – Prison-Nyakasaluma- Bunyihuna yenye urefu wa kilometa 19.46, barabara ya Ishigamva-Busabaga-Ilolangu yenye urefu wa kilometa 15 na barabara ya Ilolangu -Kisumo-Bukombe boda yenye urefu wa kilomita 17.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe, ili kuhakikisha zinapitika katika majira yote ya mwaka na kuwezesha huduma za usafiri na usafirishaji.
MHE. IDDI K. IDDI aliuliza: -

Je, lini Serikali sasa itaipandisha Halmashauri ya Wilaya ya Msalala kuwa Wilaya kamili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassim Iddi Iddi, Mbunge wa Jimbo la Msalala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa kuanzisha Mkoa na Wilaya mpya umebainishwa kupitia Sheria ya Uanzishwaji wa Mikoa na Wilaya. Kwa mujibu wa Sheria hii, utaratibu wa kuanzisha Wilaya mpya huanzia kwenye Serikali za Vijiji/Mitaa ili kupata ridhaa ya wananchi kisha hupelekwa kwenye Mabaraza ya Madiwani ya Halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC). Baada ya hatua hiyo, maombi hayo huwasilishwa Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa ajili ya uhakiki na kujiridhisha na baadaye kuwasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili akiridhia atoe kibali cha kuanzishwa kwa Wilaya husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala iko katika Wilaya ya Kahama ambayo ni moja kati ya Wilaya tano zinazounda Mkoa wa Shinyanga. Halmashauri ya Wilaya ya Msalala bado haijaanza mchakato wa kuomba kuwa Wilaya kwa kadri ya matakwa ya sheria.
MHE. OMARI M. KIGUA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga daraja linalounganisha Wilaya ya Kilindi na Kiteto kupitia Kijiji cha Sambu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA ZIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Kilindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mnadani – Sambu - Pagwi ni barabara ya mkusanyo (Collector Road) yenye urefu wa kilomita 38. Barabara hii inaanzia barabara ya TANROADS ya Kwaluguru-Songe-Kibirashi inapita katika maeneo ya Changanyikeni, Kigunga, Sambu, Makelele, Lumotio, Pagwi na kuishia katika eneo la Lugira katika Wilaya ya Kiteto ambako inaungana na barabara ya Kijungu – Sunya – Dongo katika Mkoa wa Manyara.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mpango na bajeti ya mwaka wa fedha 2021/2022 barabara hii imetengewa kiasi cha shilingi milioni 182.52 kupitia fedha za Mfuko wa Barabara (Road Fund) kwa ajili ya kufanya matengenezo ya barabara yenye urefu wa kilomita 10.5, ujenzi wa kalvati tisa na vivuko mfuto (drift)vinne.

Mheshimiwa Spika, barabara hii itaendelea kutengewa fedha kulingana na upatikanaji wa fedha kila mwaka ili kutatua changamoto iliyopo ya kutopitika kwa barabara hii.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza: -

Daraja katika barabara ya Kishanda B limefunikwa na maji, hivyo kukatisha mawasiliano ya Wananchi wa kata za Nyaruzumbura, Nyakatuntu, Kakanja, Kikukuru, Mabila na Kitwe Wilayani Kyerwa.

Je, ni lini Serikali itajenga Daraja katika barabara hiyo ili kuwarejeshea mawasiliano wananchi?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALLI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa, Innocent Sebba Bilakwate Mbunge wa Jimbo la Kyerwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kishanda B ni sehemu ya barabara ya Nyaruzumbura –Kishanda yenye jumla ya kilomita 3.4 na eneo korofi kwa maana ya tinga tinga lina urefu wa mita 300. Barabara hii ni muhimu kwa wananchi wa Wilaya ya Kyerwa kwa sababu inaunganisha Makao Makuu ya Wilaya na Kata za Nyaruzumbura, Nyakatuntu, Kikukuru, Mabira na Kitwe katika Wilaya ya Kyerwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na jiografia ya Wilaya ya Kyerwa kuwa na maeneo mengi yenye tinga tinga (swamp areas) Serikali kupitia Mfuko wa Barabara (Road Fund) imekuwa ikitenga bajeti kila mwaka kwa ajili ya ukarabati wa maeneo korofi ambapo kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2018/2019 hadi 2020/2021 shilingi milioni 862.54 zimetumika katika maeneo korofi kwa maana ya tinga tinga Wilayani Kyerwa katika barabara za Omukigando-Mkalinzi kilometa 0.18, Isingiro-Ishaka-Ibare kilometa 7.8, Nyabishenge-Nyakakoni kilomita 10, Kamuli- Mtagata-Kigorogoro (Omukagoye swamp) na barabara ya Rwabwere-Karongo kilomita 10 na utekelezaji wa barabara hii unandelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 33 kwa ajili ya ujenzi wa maboksi kalvati manne ili kusaidia kupitisha maji katika eneo la Kishanda B. Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara na madaraja nchini ikiwemo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA K.n.y. MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Suala la Vitambulisho vya ujasiriamali limekuwa ni changamoto hasa kwa Wafanyabiashara ambao wana mitaji midogo.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha au kufuta vitambulisho hivyo?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Machi 2019, Serikali kwa kuwathamini na kuwajali wajasiriamali na watoa huduma wadogo ilianzisha utaratibu wa vitambulisho ili kuwawezesha kufanya biashara katika mazingira bora na tulivu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba kweli kuna changamoto zilizojitokeza katika utoaji wa vitambulisho kwa wajasiriamali na watoa huduma wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais -TAMISEMI imefanya tathmini ya zoezi zima la ugawaji, usajili na matumizi ya vitambulisho vya wwajasiriamali na watoa huduma wadogo katika mikoa na halmashauri ili kubaini changamoto zilizopo na kufanya maboresho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia mwaka 2021 vitambulisho hivyo vimefanyiwa maboresho kadhaa ikiwemo kuwekwa picha na jina la mjasiriamali mdogo aliyepatiwa kitambulisho pamoja na ukomo wa muda wa kutumika kitambulisho hicho ambao ni mwaka mmoja tangu tarehe ya kupatiwa kitambulisho badala ya mwaka wa kalenda kama ilivyokuwa awali.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa shule za sekondari utaanza katika kata zisizo na shule za sekondari nchini ili kuendana na mpango wa Serikali wa kuhakikisha kila kata inakuwa na shule ya sekondari?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anastazia James Wambura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Elimu ya Sekondari itajenga shule mpya 1,000 za sekondari za kutwa nchini kwa kuanza na ujenzi wa shule za sekondari kwenye Kata zote ambazo hazina shule za sekondari. Mradi huo unatakelezwa kwa awamu, na katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi bilioni 220 kujenga shule 310 mpya za sekondari za kutwa nchini.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa Barabara ya Redio Habari Maalum kwenda Hospitali ya Wilaya ya Olturumet kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Redio Habari Maalum hadi Hospitali ya Wilaya ya Olturumet iliyopo Arumeru Magharibi yenye urefu wa kilomita 2.5 ni miongoni mwa miradi nchini ambayo ni ahadi za Rais. Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga barabra hiyo kwa kiwango cha lami, na itatoa kipaumbele cha ujenzi pindi fedha za ujenzi zitakapopatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuifanyia matengenezo barabara hii kila mwaka wa fedha ili kuhakikisha inapitika majira yote ya mwaka. Katika Mwaka wa Fedha 2019/2020 na 2020/2021 Serikali imetoa shilingi milioni 37.7 kwa ajili ya matengenezo ya barabara hiyo. Aidha, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 56.75 kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Redio Habari Maalum hadi Hospitali ya Wilaya ya Olturumet.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI aliuliza: -

Je, Serikali inaweza kuwahakikishia Wananchi wa Moshi Vijijini kuwa barabara za Himo – Kilema, Pofo –Mandaka, Uchira – Kisomachi na Mabogini – Kahe - Chekereni zitawekwa kwenye Bajeti ya mwaka 2021/2022 ambayo pia ni ahadi ya Mheshimiwa Rais?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara za Pofo –Mandaka – Kilema, Uchira – Kisomachi – Kolarie, Fongagate – Mabogini – Kahe na Chekereni – Kyomu – Kahe zina jumla ya urefu wa kilometa 57.28. Serikali imeendelea kujenga na kukarabati barabara hizi mwaka hadi mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali ilijenga barabara ya Uchira – Kisomachi -Kolarie kipande chenye urefu wa kilometa 1.4 kwa kiwango cha lami kwa shilingi milioni 694, ujenzi wa barabara ya Chekereni – Kyomu - Kahe kipande cha kilometa 11 kwa kiwango cha changarawe kwa gharama ya shilingi milioni 230.01 na kufanya matengenezo ya barabara za Fongagate – Mabogini - Kahe kipande cha kilometa 3 kwa gharama ya shilingi milioni 60.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2020/2021 Serikali inatekeleza kazi za matengenezo ya kawaida katika barabara ya Pofo – Mandaka – Kilema kilometa tisa kwa gharama ya shilingi milioni 13.5, matengenezo ya barabara ya Uchira – Kisomachi – Kolarie kilometa 2.5 kwa gharama ya shilingi milioni 15, matengenezo ya barabara ya Fongagate – Mabogini – Kahe kilometa mbili kwa gharama ya shilingi milioni 60 na matengenezo ya barabara ya Chekereni – Kyomu – Kahe kilomevta 3 kwa gharama ya shilingi milioni 4.5. Matengenezo ya barabara hizi yanaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 33 kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Pofo – Mandaka – Kilema kilomita 11, matengenezo ya barabara ya Uchira – Kisomachi – Kolarie kilomita 4 kwa gharama ya shilingi milioni 11 na matengenezo ya barabara ya Fongagate – Mabogini – Kahe kilomita 42.25 kwa gharama ya shilingi milioni 540.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara hizi kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itasaidia na kufanikisha kutoa Namba kwa Vijiji vya Chipunda, Mkalinda na Sululu ya Leo vyenye wakazi zaidi ya elfu kumi katika Jimbo la Ndanda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Jimbo la Ndanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vya Chipunda na Sululu ni vijiji halali ambavyo vimeendelea pia kutambulika kupitia Matangazo ya Serikali Namba 536 Mamlaka za Miji na 537 Mamlaka za Wilaya ya tarehe 19/07/2019. Vijiji hivyo pia vilishiriki kikamilifu katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika mwaka 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto ya uchakavu na upotevu wa Hati za Usajili za baadhi ya Vijiji, mwaka 2019/2020, Ofisi ya Rais – TAMISEMI ilihuisha taarifa za vijiji vyote nchini na kuandaa kanzidata ya Hati za Usajili wa Vijiji vyote nchini kwa kuzingatia matakwa ya kifungu cha 22 na 26 cha Sheria ya Serikali za Mitaa, Mamlaka za Wilaya, Sura ya 287. Hati hizo kwa sasa zipo katika hatua ya uchapishaji na zitatolewa kwa vijiji vyote nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na zoezi hilo, Kijiji cha Chipunda kilichopo Kata ya Mkululu, Halmashauri ya Wilaya ya Masasi Namba yake ya Usajili ni MTR-091-0900989. Kijiji cha Sululu kilichopo Kata ya Sululu, Halmashauri ya Mji wa Masasi Namba yake ya Usajili ni MTR-092-09011574.Kijiji cha Mkalinda hakipo katika Orodha ya Vijiji vilivyopo nchini.
MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Wilaya mpya ya Ukonga katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Ukonga liko katika Wilaya ya Ilala ambayo ni moja kati ya Wilaya tano zinazounda Mkoa wa Dar es Salaam. Utaratibu wa kuanzisha Mkoa na Wilaya mpya umebainishwa kupitia Sheria ya Uanzishwaji wa Mikoa na Wilaya Na. 397 ya mwaka 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa kuanzisha Wilaya mpya huanzia kwenye Serikali za Vijiji/Mitaa ili kupata ridhaa ya wananchi kisha hupelekwa kwenye Mabaraza ya Madiwani ya Halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC). Baada ya hatua hiyo, maombi hayo huwasilishwa Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa ajili ya uhakiki na kujiridhisha na baadaye kuwasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maamuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Ilala bado haijawasilisha maombi hayo kadri ya matakwa ya sheria.
MHE. SALIM A. HASHAM aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua changamoto ya ukosefu wa dawa na vifaa tiba katika vtuo vya kutolea huduma za afya Wilayani Ulanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salim Alaudin Hasham, Mbunge wa Jimbo la Ulanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba kwa kuongeza bajeti katika Wilaya ya Ulanga na nchini kote.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti ya dawa katika Halmashauri ya Wilaya Ulanga imeongezeka kutoka shilingi milioni 337.49 (Serikali Kuu, fedha uchangiaji huduma na Mfuko wa Pamoja wa Afya) mwaka 2015/2016 hadi shilingi milioni 475.53 mwaka 2020/2021. Upatikanaji wa dawa muhimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga umeongezeka kutoka asilimia 68 mwaka 2015/2016 hadi kufikia asilimia 82.2 mwaka 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada hizi bado kuna changamoto ya upungufu wa baadhi ya dawa na vifaa tiba vituoni. Serikali itaendelea kuboresha bajeti na usimamizi wa bidhaa hizi ili kuondoa changamoto hiyo.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa uamuzi wa mwisho wa mapendekezo ya mgawanyo wa rasilimali, madeni, majengo, watumishi na mashamba kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu na Halmashauri ya Mji wa Mbulu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu katika swali Na. 116 tarehe 12 Januari, 2021 mgawanyo wa rasilimali watu, magari, pikipiki, rasilimali na madeni kati ya Halmashauri ya Mji Mbulu na Halmashauri ya Mbulu umefanyika kwa asilimia
100 kwa kuzingatia mwongozo wa ugawaji wa mali na madeni ulioandaliwa na Ofisi ya Rais TAMISEMI wa Mwaka
2014. Katika mgawanyo huo Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu kwa maana ya Halmashauri mama, ilipata asilimia 60 na Halmashauri ya Mji wa Mbulu ilipata asilimia 40.
MHE. RASHID A. SHANGAZI K.n.y. MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA aliuliza: -

Je, Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka wa kuzipandisha hadhi barabara za ndani za Jimbo la Kawe ili zihudumiwe na TANROADS kwa kuwa uwezo wa TARURA kuhudumia ni kilometa 120 wakati Jimbo lina barabara zenye jumla ya kilometa 1,463?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Askofu Josephat Mathias Gwajima, Mbunge wa Jimbo la Kawe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la kupandisha hadhi barabara ni la kisheria na huzingatia vigezo vilivyowekwa kwa mujibu wa Sheria ya Barabara Namba 13 ya mwaka 2007 na Kanuni zake za mwaka 2009. Barabara ambayo inakidhi vigezo vya kupandishwa hadhi inatakiwa ijadiliwe kwenye Kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa husika na ikionekana inakidhi vigezo vyote Bodi ya Barabara ya Mkoa husika itamshauri Waziri mwenye dhamana na barabara kuwa barabara husika imekidhi vigezo vya kuwa na hadhi ya barabara ya Mkoa na hivyo ipandishwe daraja na kuwa barabara ya Mkoa chini ya Wakala wa Barabara Tanzania kwa maana TANROADS. Hivyo, ni vema taratibu hizo zikafuatwa ili kupandisha hadhi barabara zilizopo katika Jimbo la Kawe.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuiongezea bajeti TARURA ili kuiwezesha kuzihudumia barabara zake ikiwemo kuongeza tozo kwenye mafuta katika bajeti ya mwaka wa fedha 2021/2022 itakayowezesha TARURA kupata fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza: -

Barabara ya kutoka Ilembo hadi Itenka ni barabara muhimu kiuchumi.

Je, ni lini Serikali itaifanyia ukarabati barabara hii?

Je, ni lini sasa Serikali itaweka hela ya kutosha kuhakikisha barabara hii inakwisha kabisa kwa sasbabu ni barabara hii ya kiuchumi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa sababu kalvati kutokana na mvua nyingi zinazonyesha, makalvati haya yanachukuliwa hatimae inakuwa siyo barabara ya kalvati tena yanakuwa madaraja, na mpaka sasa hivi tunasema tumetengeneza makalvati matano, na najua si muda mrefu makalvati haya yatachukuliwa na mvua.

Je ni lini Serikali sasa itatenga pesa za kutengeneza madaraja, yapo makalvati matano sasa yatatengenezwa madaraja matano, ni lini Serikali itatoa pesa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge Jimbo la Nsimbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza alichokuwa anaomba kufahamu ni kwamba lini Serikali itatenga fedha za kutosha katika barabara hiyo ili kuhakikisha inakamilika?

Nimwambie tu kwamba Mheshimiwa Mbunge Serikali tutaendelea kuzingatia hilo ombi alilolisema lakini kwa kadri ya bajeti yetu inavyoendelea kuongezeka ndivyo tunavyoendelea kutenda fedha za kutosha kwa ajili ya barabara hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ilikuwa lini badala ya kujenga makalavati anataka tujenge madaraja katika eneo husika. Nimwambie tu kwamba sisi tunajenga kulingana na tathmini ambayo inafanywa na wakandarasi wa maeneo husika. Kwa hiyo, kama kutakuwa na hitaji la msingi la kujenga madaraja tutafanya hivyo baada ya kufanya na kupata tathmini ya kina katika barabara hiyo kuhusu hayo makalavati anayoyazungumzia Mheshimwa Mbunge, ahsante sana.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, na nataka kumpongeza Mheshimiwa Anna Lupembe kwa swali lake zuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge, mpango wetu Ofisi ya Rais - TAMISEMI kwa mwaka 2022/2023 ni kujenga madaraja na makalvati yote, kwa hiyo, sasa hivi tumeshaelekeza TARURA katika Halmashauri zote kufanya usanifu, kazi inayofanyika sasa hivi ni usanifu wa madaraja na makalvati ili tuweze kujua gharama halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tumeona tunaweze kutoa hela tukajenga barabara, lakini kama madaraja na makalvati hayajajengwa hayapitiki maana yake tumefanya kazi bure. Kwa hiyo kipaombele chetu sasa tunataka mwakani tukaelekeze kwenye madaraja na makalvati, kwa hiyo, niwatoe hofu tu waheshimiwa wabunge hili swala tumelipa kipaumbele. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa ya Kidato cha Tano na Sita katika Shule ya Sekondari Bugando iliyopo Tarafa ya Bugando na Shule ya Sekondari ya Rubanga iliyopo Tarafa ya Isulwabutundwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Jimbo la Geita, kama ifuatavyo: -

Mheshimwa Naibu Spika, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Geita pamoja na wadau wa elimu imekamilisha ujenzi wa miundombinu ya Kidato cha Tano na Sita katika Shule ya Sekondari Bugando iliyopo katika Kata ya Nzera, Tarafa ya Bugando katika Jimbo la Geita. Shule hii imepata kibali cha kuanzisha Kidato cha Tano na Sita mwaka 2021 kwa michepuo ya PCM na PCB na imepangiwa wanafunzi wa kiume 124 wataoanza kuripoti mnamo tarehe 03 Julai, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Geita inaendelea na upanuzi wa Shule ya Sekondari Lubanga iliyopo katika Kata ya Isulwabutundwe, Tarafa ya Bugando ili iweze kuwa na Kidato cha Tano na Sita. Ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa upo katika hatua ya ukamilishaji na ujenzi wa matundu 12 ya vyoo unaendelea. Halmashauri kwa kushirikiana na wadau wa elimu inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa bweni.

Aidha, Halmashauri ya Wilaya ya Geita imekamilisha ujenzi wa madarasa 4 na ununuzi wa viti 160 na meza 160 katika Shule ya Sekondari Kakubilo na inaendelea na ujenzi wa bweni na bwalo la chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya Shule za Sekondari katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita na itazipatia kibali cha kupokea wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita mara baada ya kukamilisha ujenzi wa miundombinu muhimu.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Ujenzi wa Barabara za Kwasadala – Jiweni, Mashua - Shirinjoro –Mijongweni, Kalali – Nronga, Arusha Road – Mlimashabaha –Sanya Stastesheni pamoja na Kwasadala – Uswaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara za Kwasadala –Jiweni – Mshua, barabara ya Shirinjoro – Mijengweni, barabara ya Kalali – Nronga, Arusha Road - Mlima Shabaha – Sanya Stastesheni pamoja na Kwasadala – Uswa zimesajiliwa kwa majina ya Kwasadala - Mshua yenye urefu wa kilomita 35.06, barabara ya Shirinjoro - Mijongweni yenye urefu wa kilomita 12.71, barabara ya Kalali - Nronga yenye urefu wa kilomita 6.04, barabara ya Somali - Tindigani yenye urefu wa kilomita 12.00 na Barabara ya Kwasadala - Uswaa yenye urefu wa kilomita 9.87.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali kupitia TARURA, Halmashauri ya Wilaya ya Hai imezifanyia matengenezo barabara za Kwasadala - Mashua kilomita 14, Shirinjoro - Mijongweni kilomita 5, Kalali -Nronga kilomita 5 na barabara ya Kwasadala - Uswaa kilomita 5 kwa gharama ya shilingi milioni 157.5. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga shilingi milioni 189.35 kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Kwasadala - Mshua kilomita 17, Shirinjoro - Mijongweni kilomita 4, Kalali-Nronga kilomita 5 na barabara ya Kwasadala - Uswaa kilomita 9. Matengenezo ya barabara hizo yanaendelea na yanatarajiwa kukamilika ifikapo Agosti 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 barabara hizo zimetengewa shilingi milioni 123 kwa ajili ya matengenezo ya vipande vyenye jumla ya urefu wa kilomita 30.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, ni lini jengo jipya la hospitali lililojengwa Tunduma litafunguliwa na kuanza kutoa huduma kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuboresha huduma za afya nchini kwa kutoa fedha za ukarabati na ujenzi wa vituo vya kutolea huduma za afya. Serikali imeupatia Mkoa wa Songwe kiasi cha shilingi billion 14.8 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali nne kwenye Halmashauri ya Mji wa Tunduma, Halmashauri ya Wilaya ya Songwe, Momba na Ileje.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeeendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji Tunduma ambao mpaka kukamilika inakadiriwa kugharimu shilingi bilioni 9.5. Mradi huu unatekelezwa kwa awamu mbili, ambapo awamu ya kwanza utahusisha ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD) uliogharimu kiasi cha shilingi bilioni nne. Ujenzi wa jengo hilo la ghorofa moja upo kwenye hatua ya umaliziaji. Kuanzia Julai 2021 jengo hilo lilianza kutumika kutoa huduma ya wagonjwa wa nje na kliniki ya mama wajawazito na watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Tunduma. Ujenzio huo wa majengo yatakayohusishwa ni pamoja na jengo la maabara, jengo la mionzi, jengo la huduma za dharura, jengo la afya ya kinywa na meno, macho, upasuaji na utawala.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE aliuliza: -

Je, ni lini ahadi ya Mheshimiwa Rais ya Mwaka 2015 ya ujenzi wa Kivuko cha Mto Kalambo itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephat Sinkamba Kandege Mbunge wa Jimbo la Kalambo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa ahadi ya Mheshimiwa Rais ya mwaka 2015 na vilevile ahadi ya Mheshimiwa Makamu wa Rais ya mwaka 2020 ambaye kwa sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan umeanza, ambapo upembuzi yakinifu (Detailed Design) wa kivuko hicho umekamilika mwaka 2018, ambao ulifanywa na Mhandisi Mshauri Advanced Engineering Solutions Limited ya Tanzania kwa kushirikiana na Teknicon Limited ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Kivuko hicho chenye urefu wa mita 80 unategemea kugharimu Shilingi Bilioni Nne milioni mia sita themanini na tisa mia saba themanini na tatu elfu mia saba kumi na mbili na senti hamsini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua iliyofikia sasa ni kwa Serikali kuendelelea kutafuta fedha za ujenzi wa kivuko hicho, pindi fedha zitakapopatikana ujenzi utaanza mara moja.
MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Shule ya Sekondari ya Kidato cha Tano na Sita Mungaa ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan aliyoitoa kipindi cha Kampeni mwaka 2020 alipopita Jimbo la Singida Mashariki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango wa ujenzi wa shule 26 za wasichana, moja katika kila Mkoa na ujenzi wa shule 1,000 za sekondari kwenye kata zisizo na shule za sekondari ili kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani na vikwazo hususani kwa watoto wa kike kutembea umbali mrefu. Vilevile, Serikali itafanya upanuzi wa shule za sekondari 100 kuweza kupokea wanafunzi zaidi wa kidato cha tano na sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa shule zote mpya za sekondari na upanuzi wa sekondari za kidato cha tano utafanyika kwa awamu. Awamu ya kwanza ya ujenzi itaanza mwaka wa fedha 2021/2022 ambapo Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 220. Kabla ya kuanza ujenzi, Serikali itafanya tathmini ya maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya za sekondari na mahitaji ya upanuzi wa sekondari za kidato cha tano na sita ikiwa ni pamoja na Shule ya Sekondari Mungaa.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara zinazopanda milimani Arumeru Mashariki ili kuwafikishia Wananchi huduma pamoja na kupunguza gharama za matengenezo ya mara kwa mara kwa barabara hizo ambapo gharama zake ni kubwa kutokana na ugumu wa kijiografia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali imeidhinisha jumla ya shilingi bilioni 1.93 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa barabara za milimani zenye jumla ya urefu wa kilomita 82.1 pamoja na barabara za ukanda wa chini zenye jumla ya urefu wa kilomita 22.3 kwa kiwango cha changarawe, kujenga daraja moja, makalavati 63 pamoja na kuchimba mifereji ya kuondoa maji barabarani yenye urefu wa kilomita nane.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, barabara zenye urefu wa kilomita sita za ukanda wa milimani zitafanyiwa usanifu kwa ajili ya ujenzi wa kiwango cha lami. Barabara hizo ni Leganga – Mulala kilomita mbili; Police – Magarisho kilomita mbili; Sangisi – Ndoombo kilomita mbili kwa gharama ya shilingi milioni tano kwa ajili ya usanifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2020/2021, Serikali ilifanya matengenezo ya barabara za Maji ya Chai – Sakila kilomita tatu; Police – Ngurdoto kilomita 3.5; Mji Mwema – Dispensary kilomita 0.5; Leganga – Ngarasero kilomita 0.8; Kisimiri Sekondari kilomita nne; Ngarenanyuki –Ngabobo kilomita 2.5; Ubungo – Irrikolanumbe kilomita 2.6; Sangisi – Ndoombo kilomita tano; Tengeru – Nambala kilomita mbili; Poli – Seela kilomita mbili pamoja na ujenzi wa barabara ya Sangis – Nambala kilomita 1.9 kwa kiwango cha lami kwa jumla ya gharama ya shilingi bilioni 1.38.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kwa barabara zinazopanda milimani Arumeru Mashariki kadri ya fedha zinavyopatikana.
MHE. REGINA N. QWARAY K.n.y. MHE. DANIEL B. SILLO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza mgogoro wa mpaka kati ya Kiwanda cha Mbolea cha Minjingu na Vjiji vya Olacity na Minjingu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro kati ya Kiwanda cha Mbolea cha Minjingu na Vijiji vya Olacity na Minjingu ulitokana na vijiji kutokutambua mipaka halisi kati ya vijiji hivyo na kiwanda, hivyo kusababisha wananchi kutoka katika vijiji hivyo kuingia na kufanya maendeleo katika eneo la kiwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwezi Januari, 2021 Serikali ilifanya uhakiki wa mpaka wa Kiwanda cha Minjingu na vijiji vinavyozunguka kiwanda hicho na kubaini kuwa kuna jumla ya kaya 83 ndani ya eneo la kiwanda ambapo kaya kutoka Vijiji vya Olacity na Minjingu ni miongoni mwa vijiji hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa kaya hizo, kaya 40 za wahanga wa mafuriko ambazo ziliombewa na Kijiji cha Minjingu makazi ya muda ndani ya eneo la kiwanda, lakini baada ya muda wa makubaliano kuisha, kaya hizo zimegoma kuondoka katika eneo la kiwanda, hivyo kusababisha kuwepo kwa mgogoro huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaielekeza Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Manyara kukutana na pande zote mbili zinazohusika ili kuutafutia ufumbuzi mgogoro huo ifikapo Desemba, 2021.
MHE. BENAYA L. KAPINGA aliuliza: -

Je, ni lini Vituo vya Afya vya Mapera na Muungano vitaanza kutoa huduma ya upasuaji ambao haufanyiki kutokana na kukosekana kwa baadhi ya vifaa ikiwemo sterilizer?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali katika Mwaka wa Fedha 2019/2020 iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga shilingi milioni 400 kwa ajilii ya ukarabati na upanuzi wa Kituo cha Afya Mapera ambapo ujenzi umekamilika na kituo hicho kimeanza kutoa huduma kuanzia Julai, 2021. Mpaka sasa akinamama wajawazito 11 wamekwishanufaika na huduma ya upasuaji.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Muungano kilianza kujengwa mwaka 2017 kwa nguvu za wananchi na fedha za mapato ya ndani ya halmashauri. Katika Mwaka wa Fedha 2019/2020 Serikali ilitoa shilingi milioni 60 ili kuendeleza ujenzi wa kituo hicho. Jengo la wagonjwa wa nje (OPD) limekamilika na limeanza kutoa huduma kuanzia Julai, 2021. Ujenzi wa jengo la upasuaji unaendelea na upo kwenye hatua ya ukamilishaji.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga na kukarabati vituo vya afya nchini ikiwemo Vituo vya Afya vya Mapera na Muungano ili kuboresha na kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya, dawa na vifaa tiba kote nchini.
MHE. EDWARD O. KISAU aliuliza: -

Je ni lini Serikali itapandisha hadhi Shule za Sekondari za Lesoit, Dosidosi, Ndedo na Dongo kuwa Kidato cha Tano na Sita kutokana na uhitaji mkubwa wa Shule za Kidato cha Tano na Sita Kiteto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edward Olelekaita Kisau, Mbunge wa Jimbo la Kiteto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali inatambua uhitaji mkubwa wa shule za kidato cha tano na sita katika Halmashauri ya Wilaya ya Kiteto. Shule tatu ni za bweni na moja ni ya kutwa ambazo zilianzishwa makusudi kwa ajili ya kuwasaidia ndugu zetu wafugaji wanaohamahama ili wasome bila kukatisha masomo. Shule hizo zinashindwa kupandishwa hadhi kutokana na upungufu wa miundombinu ya mabweni, mabwalo na madarasa ya kutosha kwa ajili ya kidato cha kwanza hadi cha nne na kidato cha tano na sita.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kumwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Kiteto akishirikiana na wananachi wajenge mabweni, madarasa na mabwalo kwenye shule hizo ili yatosheleze mahitaji ya wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne na kuongeza mengine ambayo yanaweza kutumika kwa ajili ya kidato cha tano na sita ili tuweze kuzipandisha hadhi shule hizo.
MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuzipandisha hadhi barabara za TARURA zinazochochea ukuaji wa uchumi kwenda TANROADS ili zipatiwe fedha za kutosha za kufanya matengenezo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu, naomba kutoa maelezo mafupi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la kupandisha hadhi barabara ni la kisheria kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa. Barabara ambayo inakidhi vigezo kutoka daraja la barabara ya wilaya kwenda daraja la barabara ya mkoa inatakiwa ijadiliwe kwenye kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa husika. Ikionekana inakidhi vigezo ndio Bodi hiyo kupitia Mwenyekiti wake itamshauri Waziri mwenye dhamana na barabara kuwa barabara husika imekidhi vigezo vya kuwa na hadhi ya Barabara ya Mkoa na hivyo ipandishwe daraja na kuwa Barabara ya Mkoa chini ya TANROADS.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la uwezo wa TARURA hususani uwezo wa rasilimali fedha, Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo, itaendelea kuiwezesha TARURA kwa kuiongezea fedha na kuijengea uwezo ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na weledi.

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza azma hiyo, katika mwaka wa fedha 2021/2022 zimetengwa shilingi bilioni 966.90 ikilinganishwa na shilingi bilioni 275.03 zilizotengwa mwaka wa 2020/2021 kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara na madaraja zinazosimamiwa na TARURA.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Daraja la Gunyoda ambalo linaunganisha Halmashauri ya Mji wa Mbulu, Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu na Halmashauri ya Wilaya ya Karatu hususani Tarafa ya Mang’ola kwenye mashamba ya vitunguu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekwishachukua hatua za kufanya upembuzi wa awali kwenye Korongo la Gunyoda lililoko katika Barabara ya Waama-Masieda, Kata ya Gunyoda katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu ambako ndiko daraja hilo litajengwa. Korongo hilo lina urefu wa mita 70.4 na kina cha mita 5.0. Kutokana na ukubwa wa korongo hilo, upembuzi ulibainisha kuwa, ili kujenga Daraja la Gunyoda zinahitajika shilingi bilioni 1.2. Fedha hizi ni zaidi ya ukomo wa bajeti ya Halmashauri katika Fedha za Mfuko wa Barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kwa kuona umuhimu wa daraja la Gunyoda ikizingatiwa daraja hilo linaunganisha Halmashauri ya Mji wa Mbulu, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuhakikisha daraja hilo linajengwa kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. JACQUELINE K. ANDREA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Zahanati katika Kata ya Ng’ambo iliyopo Tabora Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Andrea Kainja Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma ya zahanati kwa fedha kutoka Serikali kuu na fedha za makusanyo ya ndani ya Halmashauri. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetoa fedha shilingi bilioni 27.75, kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati 555. Ambapo Halmashauri ya Manispaa ya Tabora ilipokea fedha ya shilingi milioni 150, kwa ajili ya ukamilishaji wa Zahanati ya Ituru, Igosha na Igombe.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 35.15, kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati 758 nchi nzima. Ambapo Halmashauri ya Manispaa Tabora imetengewa shilingi milioni 100 kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya Zahanati ya Zaire na Zahanati ya Kapunze kila moja shilingi milioni 50. Aidha, kupitia mapato ya ndani Manispaa ya Tabora imetenga fedha shilingi milioni 100 kwa ajili ya kukamilisha zahanati ya Mtendeni na Zahanati ya Igambilo, kila moja kwa shilingi milioni 50.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati yaliyojengwa na wananchi kote nchini. Aidha, Halmashauri ya Manispaa ya Tabora inashauriwa kutenga fedha kutoka katika mapato ya ndani kwa ajili ya kuanza ujenzi wa zahanati katika Kata ya Ng’ambo ili kusogeza huduma kwa wananchi.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa kipaumbele wa kuongeza mtandao wa barabara za lami za Mji Mkongwe na wakitalii wa Mbamba Bay?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Stella Martin Manyanya Mbunge wa Jimbo la Nyasa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Barabara Vijijini na Mjini (TARURA) inaendelea na ujenzi wa lami kilometa moja unaogharimu jumla ya shilingi milioni 473.50 unaotekelezwa na Mkandarasi VAG Contractors Ltd. katika eneo la Makao Makuu ya Wilaya kwa maana ya Bomani kwa mwaka wa fedha 2021/2022 pamoja na ujenzi wa kilometa 0.5 Kata ya Kilosa katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa eneo la Mbamba Bay kama eneo la utalii na shughuli za Uvuvi. Hivyo, Serikali itaendelea kutenga fedha kujenga barabara kwa kiwango cha lami kulingana na upatikanaji wa fedha katika eneo la Mbamba Bay.
MHE. TABASAM H. MWAGAO aliuliza: -

Je, mpango wa kuzipandisha hadhi Sekondari za Ngweli, Ngoma A, Tamabu, Nyamatongo, Sima, Nyampande na Katunguru kuwa za Kidato cha Tano na Sita Wilayani Sengerema umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tabasam Hamis Mwagao Mbunge wa Jimbo la Sengerema, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa spika, kabla ya shule kusajiliwa Kidato cha Tano na Sita inatakiwa kuwa na miundombinu ya msingi kwa ajili ya kupokea wanafunzi. Jukumu la ujenzi wa miundombinu hiyo si la Serikali kuu tu bali ni la halmashauri kupitia mapato yake ya ndani pamoja na wadau wa elimu na jamii nzima kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, namshauri Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na Mkurugenzi wa Halmashuri ya Wilaya Sengerema na kuwasiliana na Ofisi ya Uthibiti Ubora kufanya tathmini katika Shule za Sekondari za Ngweli, Ngoma A, Tamabu, Nyamatongo, Sima, Nyampande na Katunguru ili kujiridhisha na hali ya miundombinu ya msingi kwa ajili ya kupokea wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga miundombinu katika baadhi ya shule zilizopendekezwa kuanzisha Kidato cha Tano na Sita kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha ili kuongeza fursa ya Elimu.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya kutoka Kalambo Falls hadi barabara kuu inayokwenda Matai yenye urefu wa kilometa17?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa ukarabati wa barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 17 kwa kiwango cha Changarawe unaendelea ambapo kwa mwaka wa fedha 2020/2021, Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa Halmashauri ya Wilaya Kalambo kwa kushirikana na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kwa maana ya TFS ulitumia kiasi cha shilingi milioni 139.72 kukarabati sehemu ya barabara hiyo kipande chenye urefu wa Kilometa 10.

Mheshimiwa Spika, vile vile kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Halmashauri ya Wilaya Kalambo umetenga kiasi cha shilingi milioni 84.5 kwa ajili ya matengenezo ya muda maalum kwa maana Periodic Maintenance kipande chenye urefu wa kilometa 4 na Mkandarasi amekwisha patikana na yupo eneo la mradi akiendelea na kazi.

Mheshimiwa Spika, hali ya barabara hii kwa sasa inaridhisha kwani inapitika katika kipindi chote cha mwaka. Aidha, kutokana na umuhimu wa barabara hii, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya matengenezo yake kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. ERIC J. SHIGONGO K.n.y. MHE. SALMA R. KIKWETE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga kivuko kutoka Mchinga Moja kwenda Mchinga Mbili ili kurahisisha huduma kwa wananchi ikiwemo wanafunzi wanaovuka bahari kwa miguu kwenda Shule ya Sekondari Mchinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete, Mbunge wa Jimbo la Mchinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa changamoto ya kivuko katika barabara ya Mchinga –Kijiweni, eneo la kutoka Mchinga Moja kwenda Mchinga Mbili lililo katika Jimbo la Mchinga, Wilaya ya Lindi. Serikali kupitia TARURA Mkoa wa Lindi, imeshafanya tathimini ya awali ya kutatua changamoto hiyo ambapo kiasi cha shilingi milioni 147 kitaweza kujenga kivuko cha waenda kwa miguu (pedestrian suspended bridge).

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023 TARURA Wilaya ya Lindi itatenga bajeti ya kiasi cha shilingi milioni 147 kwa ajili ya kujenga kivuko cha waenda kwa miguu. Aidha, ujenzi wa kivuko hicho utaondoa changamoto ya usafiri na usafirishaji katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara katika Jimbo la Mchinga kulinga na upatikanaji wa fedha.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga wodi mpya ya akinamama Wilayani Mbozi itakayokuwa na nafasi ya kutosha kwa ajili ya akinamama wengi kujifungua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali Mpya ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe itakayogharimu jumla ya shilingi bilioni 12.26 mpaka kukamilika kwake. Hadi kufikia Disemba 2021 shilingi bilioni 9.8 imetolewa, ambapo jengo la OPD limekamilika na ujenzi wa wodi ya mama na mtoto unaendelea na unatarajiwa kukamilika Disemba, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga Shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Mbozi ambayo kwa sasa inatumika kama Hospitali Teule ya Mkoa wa Songwe.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza: -

Je ni lini serikali itajenga madaraja ya Gunyoda na Baray ikizingatiwa kuwa madaraja haya ni muhimu sana katika kuunganisha Halmashauri ya Mji wa Mbulu, Halmashauri ya wilaya ya Mbulu na Karatu?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Korongo la Gunyoda lenye urefu wa mita 70.4 na kina cha mita tano lipo barabara ya Waama-Masieda katika ya kata ya Gunyoda, Halmashauri ya Mji wa Mbulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kutokana na umuhimu wa daraja la Gunyoda ambalo linaunganisha Halmashauri za Wilaya ya Mbulu, Karatu na Halmashauri ya Mji wa Mbulu, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini imetetenga bajeti katika mwaka wa fedha wa 2022/2023 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu ili kufahamu gharama halisi zinazohitajika katika ujenzi wa daraja hilo. Baada ya kukamilika kwa upembuzi na usanifu wa barabara hiyo, Serikali itatafuta fedha kutoka vyanzo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali imekuwa ikifanya matengenezo ya barabara ya Waama – Masieda yenye urefu wa kilomita 19.98 lenye korongo la Gunyoda ambapo katika mwaka wa fedha 2020/2021 jumla ya kilometa 17.25 za barabara zilifanyiwa matengenezo kwa shilingi milioni 70.25. Kwa upande wa mwaka wa fedha 2021/ 2022 jumla ya kilometa 14.2 zitatengenezwa kwa shilingi milioni 34.22 na Mkandarasi ameanza kazi za matengenezo na zitakamilika mwezi Mei, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya barabara katika Jimbo la Mbulu kulingana na upatikanaji wa fedha, ili kuimarisha upatikanaji wa huduma muhimu za jamii na kiuchumi.
MHE. DEO K. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kujenga kilomita sita ya barabara kwa kiwango cha lami katika Mji wa Makambako?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zilizoahidiwa zinasimamiwa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini kwa maana ya TARURA. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano aliahidi kujenga kilomita sita za barabara kwa kiwango cha lami katika Halmashauri ya Mji wa Makambako ambapo Wakala wa Barabara TANROADS alikasimiwa kutekeleza ujenzi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia mwaka wa fedha 2020/2021, jumla ya kilomita 3.5 zimejengwa kwa kiwango cha lami ambapo jumla ya Shilingi bilioni 1.97 zilitumika katika ujenzi huo. Aidha, Serikali itaendelea kutenga fedha ili kukamilisha ujenzi wa kilomita sita kwa kiwango cha lami kwa kadri fedha zitakavyopatikana. Ahsante sana.
MHE. BENAYA L. KAPINGA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga daraja linalounganisha Vijiji vya Kingoli – Litumbandyosi Wilaya ya Mbinga na Machimavyalafu Wilaya ya Ludewa katika Mto Ruhuhu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Liuka Kapinga Benaya, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, daraja la kuunganisha Vijiji vya Kingoli – Litumbandiyosi ni moja kati ya madaraja makubwa ambayo yamepewa kipaumbele na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kingoli hadi mto Ruhuhu yenye urefu wa kilometa 13.0 kwa sasa haipitiki kutokana na kukosekana kwa madaraja madogo ya kudumu katika Mito ya Linyanya na Nyamilola pamoja na daraja kubwa la Mto Ruhuhu. Hata hivyo, TARURA Wilaya ya Mbinga, ilitenga fedha katika Bajeti ya Mwaka wa fedha 2021/2022 ili kujenga madaraja mawili madogo ya Linyanya na Nyamilola na sasa hivi mkandarasi yuko anaendelea na kazi ya ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uhitaji mkubwa wa madaraja katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga na kwa kuzingatia umuhimu wa daraja linalounganisha Mkoa wa Ruvuma na Njombe kupitia vijiji vya Kingoli – Litumbandiyosi, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini itatenga shilingi milioni 25 katika bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023 kwa ajili ya kufanya usanifu wa daraja linalounganisha Mikoa ya Ruvuma na Njombe lisilopungua urefu wa mita 40 ili kujua gharama halisi na ujenzi wake utaanza kulingana na upatikanaji wa fedha kuanzia bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024. Ahsante.
MHE. YAHYA A. MHATA K.n.y. MHE. MAIMUNA S. MTANDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ukarabati wa shule za msingi kongwe ambazo zimechakaa na majengo yake ni mafupi ulikinganisha na yanayojengwa kwa sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maimuna Salum Mtanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uwepo wa shule kongwe za msingi zilizo katika hali ya uchakavu. Kazi ya kuzikarabati shule hizi ilishaanza kupitia miradi mbalimbali ya elimu.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuboresha miundombinu ya elimu kwa kujenga na kukarabati miundombinu mbalimbali ya shule za msingi nchini. Katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali kupitia Programu ya EP4R (Lipa Kulingana na Matokeo) imeendelea na ujenzi wa vyumba vya madarasa ya shule za msingi 1,970, matundu ya vyoo 5,303, nyumba za walimu wa msingi 17. Ujenzi huu ni kwa ajili ya kuboresha mazingira ya miundombinu ya shule za msingi zikiwemo shule kongwe ambazo zina miundombinu chakavu. Vilevile kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19 (TCRP), Serikali imejenga vyumba 3,000 vya madarasa katika vituo shikizi 970.

Mheshimiwa Spika Serikali kupitia Mradi wa BOOST utakaotekelezwa katika shule za msingi inatarajiwa kujenga madarasa 12,000 katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 na itaendelea kutumia fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri kujenga na kukarabati shule za msingi kongwe nchini.
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO aliuliza: -

Je, nini hatma ya wananchi wa Ubungo Kisiwani waliofanyiwa tathmini ya kulipwa fidia ili wapishe ujenzi wa mradi wa mabasi yaendayo kasi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Kitila Alexander Mkumbo, Mbunge wa Jimbo la Ubungo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, eneo la makazi ya watu la Ubungo Kisiwani lilifanyiwa uthamini na kuandaa jedwali la uthamini lililothibitishwa na kusainiwa na Mthamini Mkuu wa Serikali mwezi Aprili, 2022 lenye jumla ya Shilingi bilioni 7.87 zitakazolipwa kwa wananchi 90 wa eneo hilo watakaopisha ujenzi wa Karakana hiyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kulipa fidia hiyo kwa wananchi 90 na mara zinakapopatikana malipo hayo yatafanyika.
MHE. ESTHER E. MALLEKO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza mkakati wa ujenzi wa hosteli kwenye shule za kata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa shule kuwa karibu na jamii na kwa muktadha huo Serikali ilielekeza kujengwa kwa shule za kata nchi nzima ili kuwawezesha wanafunzi kusoma karibu na maeneo wanayoishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu uliopo kwa sasa wa ujenzi wa hosteli kwenye shule za kata ambazo kulingana na jiografia ya eneo hususani umbali kutoka shule na makazi ya watu wananchi wenyewe wamekuwa wakijenga hosteli hizo na kuweka utaratibu wa kuziendesha na kuzisimamia kulingana na mahitaji waliyonayo.
MHE. JERRY W. SILAA K.n.y. MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE aliuliza: -

Je, ni lini Mradi wa Dar es Salaam Metrpolitan Development Project awamu ya pili utaanza katika Jimbo la Kigamboni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Faustine Engelbert Ndugulile, Mbunge wa Jimbo la Kigamboni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kufanya mazungumzo na Benki ya Dunia juu ya mkopo wa fedha kwa ajili ya Mradi wa Uboreshaji wa Miundombinu katika Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP) ambapo Halmashauri zote za Mkoa wa Dar es Salaam zitanufaika pamoja na Jimbo la Kigamboni. Aidha, maandalizi ya mradi huo yanategemewa kuanza mwezi Januari, 2023.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kutekeleza mradi wa ujenzi wa soko kuu na stendi ya mabasi Lindi Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Jimbo la Lindi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imejumuisha mradi wa soko kuu na stendi kwenye Mpango wa TACTIC unaojumuisha Halmashauri 45 ambapo Halmashauri ya Manispaa ya Lindi ipo katika awamu ya pili ya utekelezaji wa mradi huo inayohusisha Halmashauri 15 zinazotarajiwa kuanza Januari, 2023.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupandisha hadhi barabara ya Tunduru – Namasakata – Misechela kuwa ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Barabara Na. 13 ya Mwaka 2007 na Kanuni zake za Mwaka 2009, imeainisha vigezo na utaratibu wa kupandisha au kuteremsha hadhi barabara toka daraja moja kwenda daraja lingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inaielekeza Halmashauri ya Wilaya Tunduru kupitia TARURA kufuata utaratibu huo ili kuiweka barabara hiyo katika mpango wa kupandishwa hadhi na kuwa ya Mkoa.
MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza: -

Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya sintofahamu ya utaratibu wa kuwapata wanafunzi wanaorudishwa masomoni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetoa Mwongozo wa Februari, 2022 wa kuwarejesha wanafunzi waliokatisha masomo katika elimu ya msingi na sekondari kwa sababu mbalimbali ili waweze kukamilisha mzunguko wa elimu katika ngazi husika.
MHE. JONAS V. ZEELAND aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kumaliza barabara ya Manyinga hadi Madizini kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais -TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas Van Zeeland Mbunge wa Jimbo la Mvomero, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali ilitenga fedha kiasi cha shilingi milioni 500.00 kwa ajili ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kwa urefu wa kilomita 0.54 ambapo ujenzi huo umekamilika.

Mheshimiwa Spika, TARURA itaendelea na ukamilishaji wa kipande kilichobaki kulingana na upatikanaji wa fedha ili wananchi wa eneo la Madizini na sehemu zingine katika tarafa ya Turiani waweze kufanya shughuli zao za kijamii na kiuchumi kwa ufanisi.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga shule mpya za msingi katika maeneo ya Mbirani, Makibo, Kiyombo na Tutuo – Sikonge?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI inakamilisha tathmini ya upembuzi yakinifu wa Shule zote za msingi kupitia mradi wa Boost ili kubaini taarifa za eneo shule ilipo, hali ya mazingira shule ilipo, umbali kutoka shule moja hadi nyingine, umbali kati ya shule na makazi ya watu na idadi ya watu (School Mapping). Lengo lake likiwa ni kuandaa mpango endelevu wa uboreshaji wa elimu nchini.

Mheshimiwa Spika, baada ya uhuishaji huo, kwa mwaka wa fedha 2022/2023 kupitia mradi wa Boost Serikali imetenga Shilingi Bilioni 230 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya shule za msingi katika Halmashauri zote 184 ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge.
MHE. JAFARI W. CHEGE aliuliza: -

Je, ni lini Mamlaka ya Mji Mdogo Shirati katika Wilaya ya Rorya itaanza kufanya kazi kama Mamlaka kamili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Mji Mdogo wa Shirati itaanza mara baada ya Halmashauri mama ya Rorya kukamilisha mchakato wake wa kukusanya na kuimarisha mapato ya ndani ili iweze kuzihudumia Halmashauri mama na Mamlaka ya Mji mdogo wa Shirati.
MHE. DOROTHY G. KILAVE aliuliza: -

Je ni lini Serikali itamaliza mgogoro wa Ardhi kati ya Wananchi na Serikali katika Kata ya Yombo Vituka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Dorothy George Kilave, Mbunge wa Jimbo la Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mgogoro wa ardhi baina ya wananchi na Serikali ili kupisha ujenzi na upanuzi wa Shule ya Msingi Uwanja wa Ndege, ulihitimishwa tarehe 26 Septemba, 2022 baada Mahakama ya Rufaa kutupilia mbali Shauri la Rufaa Na. 116/2019 lililofunguliwa na walalamikaji 56 ambao walishindwa kuthibitisha madai yao.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kujenga Daraja Kata ya Arusha chini litakalounganisha Vijiji vya Muungano, Mikocheni na Chemchem?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prof. Patrick Alois Ndakidemi, Mbunge wa Jimbo la Moshi Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 barabara hii imetengewa fedha kiasi cha Shilingi milioni 475.00 kwa ajili ya kuanza kujenga daraja katika Mto Ronga ili kuweza kuunganisha Vijiji vya Muungano, Mikocheni na Chemchem. Mradi huu upo katika hatua za manunuzi kwa ajili ya kumpata Mkandarasi.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TARURA itaendelea kuweka katika vipaumbele vyake ujenzi wa barabara hii kulingana na upatikanaji wa fedha ili kuhakikisha inaweza kupitika katika kipindi chote cha mwaka.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati wa kukarabati barabara zilizo katika hali mbaya Wilayani Kyela kwani bajeti ya TARURA haitoshi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Ally Anyigulile Jumbe Mlaghila, Mbunge wa Jimbo la Kyela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kunusuru barabara ambazo zipo katika hali mbaya sana Wilayani Kyela, Serikali imeweka mikakati ifuatayo: -

(i) Kuzipandisha hadhi barabara za udongo kwenda changarawe (Gravel standard);

(ii) Kuzipandisha hadhi barabara za changarawe kuwa barabara za lami;

(iii) Kuendelea kuongeza fedha kwa ajili ya matengenezo na ukarabati wa barabara, mfano, bajeti ya TARURA Kyela kwa mwaka 2020/2021 ilikuwa Sh.611,136,079.47; mwaka 2021/2022 bajeti ya Kyela ilikuwa ni Sh.2,436,996,341.18; na

(iv) Kuendelea kutoa fedha za dharura kunusuru barabara zilizoathiriwa na mvua, mfano, katika mwaka 2021/2022 zimepelekwa milioni 901.52.

Mheshimiwa Spika, fedha zinazopelekwa kwa maelekezo maalum ni kwa ajili ya kutatua changamoto za muda mfupi za barababara zilizoathiriwa na mvua ili ziweze kupitika kwa wakati huo.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je, ni lini Barabara ya kutoka Igalukilo - Sayaka inayounganisha Mikoa ya Mwanza na Simiyu itahamishiwa TANROADS?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Barabara, Namba 13 ya mwaka 2007 na Kanuni zake za mwaka 2009, imeainisha vigezo na utaratibu wa kuhamisha barabara ili iwe chini ya TANROADS ambapo barabara inaweza kupandishwa au kuteremshwa toka daraja moja kwenda daraja lingine.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inaielekeza Halmashauri ya Wilaya Busega kupitia TARURA kufuata utaratibu huo ili kuiweka barabara hiyo katika mpango wa kupandishwa hadhi na kuwa ya mkoa.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga uzio na uwanja wa michezo katika Shule Maalum ya Watoto wa kike Asharose migiro iliyopo Wilayani Mwanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena Athuman Bushiri, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa michezo na utamaduni katika ukuaji na maendeleo ya wanafunzi na kutazama michezo na sanaa kwa mlengo wa ajira na stadi muhimu zinazochangia ukuaji wa kiuchumi na kijamii, Serikali imedhamiria kuboresha miundombinu ya michezo katika Shule teule 56 nchini ikiwa ni wastani wa shule mbili kwa kila mkoa.

Mhesahimiwa spika, Shule ya Sekondari Asharose Migiro haipo kwenye mpango wa shule za sekondari zilizochaguliwa kuwa za michezo hivyo, inashauriwa Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga kutenga fedha kwenye Bajeti yake ya mapato ya ndani ili kuanza ujenzi wa uzio katika viwanja hivyo.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI aliuliza: -

Je, ni nini kinakwamisha barabara ya Magamba – Mtapenda – Kasokola hadi Ifukutwa kuhamishiwa TANROADS?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Magamba – Mtapenda - Kasokola hadi Ifukutwa ni mojawapo ya barabara iliyopendekezwa na Kikao cha Kumi na Nane cha Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Katavi kilichofanyika tarehe 23 Februari, 2022 kupandishwa hadhi kuwa barabara ya Mkoa.

Mheshimiwa Spika, Mwenyekiti wa Kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Katavi kwa maana ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi alimwandikia barua Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi barua yenye Kumb. Na FA.364/423/01“C”/29 ya tarehe 11 Oktoba, 2022 kuomba kibali cha kupandishwa hadhi barabara za Wilaya ikiwemo barabara ya Magamba – Mtapenda - Kasokola hadi Ifukutwa kuwa barabara za Mkoa. Mkoa utajulishwa na Waziri mwenye dhamana na barabara kupitia Gazeti la Serikali endapo imekidhi vigezo.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali kupitia TARURA tutaendelea kuihudumia barabara hii kwa kutenga fedha kwenye bajeti zetu ili iweze kupitika muda wote kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kusambaza vipimo vya maabara hasa vya malaria katika zahanati za Mtwara Vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shamsia Azizi Mtamba, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Septemba, 2022, kipimo cha Malaria (mRDT), kuna vitepe vya kutosheleza matumizi ya miezi mitano na kabla ya kufika tarehe 30 Desemba, 2022 Bohari Kuu ya Dawa inategemea kupokea shehena nyingine ya vitendanishi hivyo vya malaria. Aidha, hali ya upatikanaji wa vitendanishi vya vipimo vya malaria katika Kanda ya Mtwara kufikia Oktoba, 2022 ni vitepe 631,825 ukilinganisha na matumizi ya vitepe hivyo ambavyo ni 84,150 kwa mwezi katika Kanda ya Mtwara, hivyo kuna shehena ya kutosheleza miezi saba ijayo.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inaendelea kuwakumbusha watumishi wanaohusika kuandaa taarifa na kuomba vitendanishi kwa ajili ya vipimo hivyo, kufanya maoteo kwa usahihi na kuomba kwa wakati maana vitendanishi hivyo vipo vya kutosha MSD Makao Makuu na kwenye Kanda husika.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA aliuliza: -

Je, ni lini wananchi wa Ifakara watapewa fedha za ujenzi wa Soko la Halmashauri ya Mji wa Ifakara ambao umesuasua kwa muda sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abubakari Damian Asenga, Mbunge wa Jimbo la Kilombero kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara kuwa na Soko la Kisasa ili kuboresha mazingira ya wafanyabishara wa Mji wa Ifakara na kuongeza mapato ya Halmashauri hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Mji wa Ifakara iliandaa na kuwasilisha Serikali Kuu andiko la mradi wa kimkakati wa ujenzi wa soko hilo kwa gharama ya shilingi bilioni 14.3 ambalo halikukidhi vigezo. Hivyo, Halmashauri ya Mji wa Ifakara inahimizwa kuweka kipaumbele na kutenga fedha kwenye bajeti yao ili kukamilisha andiko la mradi huo ambalo litawezesha kutafauta fedha za kutekeleza mradi huo.
MHE. KUNTI Y. MAJALA K.n.y. MHE. STELLA S. FIYAO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Ivuna hadi Chole ili kurahisisha mawasiliano kati ya Wilaya ya Momba na Songwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Simon Fiyao, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Ivuna hadi Chole yenye urefu wa kilomita 18.5 ni barabara muhimu iliyopo Wilaya ya Momba ambayo inaungainisha barabara ya Muheza hadi Isanzu yenye urefu wa kilomita 12 katika Wilaya ya Songwe. Ili kuunganisha Wilaya hizi mbili jumla ya kilometa 30.50 zinatakiwa kufanyiwa matengenezo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/ 2023, Serikali itatenga jumla ya Shilingi Milioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa daraja lenye urefu wa mita 200 katika barabara ya Ivuna – Chole Wilaya ya Momba na kwa upande wa Wilaya ya Songwe Shilingi Milioni 100 kwa ajili ya kufanya matengenezo yenye urefu wa kilomita 3 katika barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya barabara katika barabara hii yenye urefu wa kilometa 30.5 kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha Kituo cha Afya Kiloleli pamoja na kupeleka Vifaa kwenye Hospitali ya Wilaya Busega?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Kiloleli kilipandishwa hadhi kutoka Zahanati kuwa Kituo cha Afya mwaka 2016. Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya Kituo hicho ambapo jumla ya shilingi milioni 57 zilipelekwa katika mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya kujenga Wodi ya Wazazi na ujenzi wa Jengo la stoo ya dawa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 shilingi milioni 90 zimepelekwa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya watumishi, kwa maana ya three in one, ujenzi ambao upo katika hatua ya msingi. Mpango wa Serikali ni kuendelea kutenga fedha kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, Serikali imetenga shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya unununuzi wa vifaa tiba kupitia Bohari Kuu ya Dawa. Tayari baadhi ya vifaa tiba vimeshapelekwa kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Busega. Ahsante sana.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itasaidia ujenzi wa Stendi ya Madaba ikizingatiwa kwamba stendi hiyo ipo kwenye eneo la kimkakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Joseph Kizito Mhagama, Mbunge wa Jimbo la Madaba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Madaba kuwa na stendi ya mabasi katika Mji wa Madaba ili kuboresha upatikanaji wa huduma na kuongeza mapato ya Halmashauri hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Madaba katika mwaka wa fedha 2018/2019 iliandaa na kuwasilisha Serikali Kuu andiko la Mradi wa Kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa stendi ya mabasi ambalo halikukidhi vigezo. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Halmashauri ya Wilaya ya Madaba imepanga kutumia Shilingi Milioni Tano, kwa ajili ya kukamilisha upembuzi yakinifu (feasibility study) kwa ajili maandalizi ya andiko la mradi wa ujenzi wa stendi litakalowasilishwa Serikali Kuu ili iweze kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo wa kimkakati.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Waziri Mkuu aliyoitoa mwaka 2017/2018 ya Ujenzi wa Kituo cha Afya Ulowa katika Jimbo la Ushetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Peter Cherehani, Mbunge wa Jimbo la Ushetu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutekeleza ahadi mbalimbali zinazotolewa na viongozi wa Kitaifa kote nchini ikiwemo ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika jimbo la Ushetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 inaendelea na mpango wa kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati yenye uhitaji mkubwa nchini kote ikiwemo Kituo cha Afya cha Ulowa.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka Watumishi wa Afya wa Kada mbalimbali katika Wilaya ya Kakonko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Jimbo la Buyungu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali iliajiri Watumishi wa kada za afya 2,726 ambapo Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko ilipelekewa watumishi 24 waliopangwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imepanga kuajiri watumishi wa kada mbalimbali za afya kwa ajili ya kuboresha hali ya utoaji huduma za afya nchini kote ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na wadau itaendelea na mpango wa kuajiri watumishi wa kada za afya kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA K.n.y. MHE. SALMA R. KIKWETE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya ujenzi wa barabara ya Moka-Mtumbikile - Matimba kwa kiwango cha changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete Mbunge wa Jimbo la Mchinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) ilitenga Shilingi milioni 622.52 kwa ajili ya ujenzi wa vented drift yenye urefu wa Mita 45 na upana wa mita 7; ujenzi wa boksi kalavati kubwa katika mto Nangaru lenye urefu wa mita 26.8 na upana wa mita tisa; Kuchonga barabara yenye urefu wa kilomita 10.3, Kuweka changarawe kilomita mbili na kuchimba mifereji ya kuondoa maji barabarani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TARURA itajenga barabara ya Moka-Mtumbikile-Matimba kwa kiwango cha changarawe kadri ya upatikanaji wa fedha baada ya kukamilisha ujenzi wa vikwazo (Bottlenecks) vya barabara hiyo.
MHE. SANTIEL E. KIRUMBA aliuliza: -
Je, Serikali haioni haja ya kujenga vyoo maalum kwa ajili ya wanafunzi wa kike katika madarasa mapya yanayojengwa ili wanafunzi hawa wasikose masomo pindi wanapokuwa kwenye siku zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Santiel Erick Kirumba Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa matundu ya vyoo unazingatia mahitaji ya wamafunzi wote wakiwemo wavulana na wasichana pamoja na wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuzingatia hili Ofisi ya Rais-TAMISEMI itaendelea kuzisimamia na kuzielekeza Mamlaka za Serikali za Mitaa pindi wanapojenga shule
mpya wazingatie kujenga matundu ya vyoo kulingana na michoro na ramani zote zinazotumwa kwao kwa kuwa ndani ya michoro hiyo imejumuisha chumba maalum cha wasichana kwa ajili ya kujisitiri wanapokuwa katika hedhi.
MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga nyumba za Walimu katika Halmashauri ya Ikungi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA(MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Tais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu Mbunge wa singida Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya mahitaji ya Nyumba za Walimu Nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya Ikungi.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Ikungi ina mahitaji ya nyumba 454 na nyumba zilizopo ni 172, ili kukabiliana na upungufu uliopo kwa mwaka wa fedha 2022/2023 Halmashauri ya Wilaya Ikungi imetenga Shilingi Milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba nne za Walimu katika shule za Mandigu Kata ya Munga, Nali - Kata ya Siuyu, Mankumbi - Kata ya Kikio na Mau - Kata ya Ikungi.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu kwa Halmashauri ikiwemo na Halmashauri ya Ikungi kadri fedha zitakavyopatikana.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga kwa kiwango cha lami barabara inayoanzia Mji wa Kakonko hadi Muhange?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Jimbo la Buyungu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kakonko kupitia Vijiji vya Kinonko, Ruhuru, Nyakiyobe, Gwarama, Kabane hadi Muhange inasimamiwa na mamlaka mbili kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kipande cha barabara kutoka Kakonko – Kinonko – Ruhuru – Nyakiyobe – Gwarama yenye urefu wa kilometa 26 inasimamiwa na TANROADS na kipande cha barabara kutoka Gwarama – Muhange yenye urefu wa kilomita nane inasimamiwa na TARURA.

Mheshimiwa Spika, kipande cha barabara inayosimamiwa na TARURA yenye urefu wa kilomita nane ipo katika hali nzuri kufuatia matengenezo yaliyofanyika katika mwaka wa fedha 2019/2020 kwa gharama ya shilingi milioni 40.88.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, kipande cha barabara hii yenye urefu wa kilomita tano, kiasi cha shilingi milioni 10 imetengwa kwa ajili ya matengenezo ili kuhakikisha huduma za kiuchumi na kijamii zinaendelea kufanyika kwa wananchi kwa kipindi chote cha mwaka.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara za Jimbo la Buyungu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa vya maabara kwa wanafunzi wa masomo ya sayansi katika shule za sekondari katika Jimbo la Mbozi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Ranwell Mwenisongole, Mbunge wa Jimbo la Mbozi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikipeleka fedha katika shule za sekondari kwa ajili ya umaliziaji wa miundombinu mbalimbali ikiwemo maabara za masomo ya sayansi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2022/2023 Serikali imetenga Shilingi bilioni 5.14 kupitia Programu ya SEQUIP kwa ajili ya kununua vifaa vya maabara kwa shule 234 za Sekondari za Kata. Hata hivyo, Serikali kwa mwaka wa fedha 2020/2021 na 2021/2022 imepeleka vifaa vya maabara katika shule za sekondari 1,258 nchini zilizokamilisha ujenzi wa vyumba vya maabara zikiwemo shule 12 za sekondari za Wilaya ya Mbozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kugawa vifaa hivyo nchini ikiwa ni pamoja na shule za Wilaya ya Mbozi kwa kuzingatia mahitaji na upatikanaji wa fedha na wadau mbalimbali.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA K. n. y. MHE. JACQUELINE K. ANDREA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Shule nyingine ya Msingi katika Kata ya Ng’ambo Tabora Mjini kwani Kata hiyo ni kubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Andrea Kainja Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli shule nyingi za msingi hapa nchini zina wanafunzi wengi wanaozidi kiwango katika shule. Hali hiyo pia ni matokeo ya utekelezaji wa Sera ya Elimu Msingi bila malipo iliyoanza utekelezaji wake mwaka 2016.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata Ng’ambo ina shule moja ya msingi yenye madarasa 17 ambayo yanahudumia wanafunzi 2,408. Aidha, ili kukabiliana na ongezeko la wanafunzi katika Kata hiyo Halmashauri ya Manispaa ya Tabora kwa mwaka wa fedha 2022/2023 imetenga Shilingi Milioni 50 za mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi madarasa mawili ya shule mpya ya msingi inayotarajiwa kujengwa katika eneo la Kilimani katika Kata hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 itatenga fedha ya ujenzi wa madarasa katika shule mpya ya msingi eneo la Kilimani kupitia programu ya EP4R.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga njia mbili katika barabara ya Bandarini hadi Rwamishenye na CRDB mpaka Njiapanda ya Kashai ili kuondoa msongamano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Bandarini – Rwamishenye yenye urefu wa kilomita 4.6 inafanyiwa usanifu wa kina ulioanza tarehe 22 Machi, 2022 kwa ajili ya kuwa Barabara ya njia mbili. Kazi ya usanifu inafanywa na Mhandisi Mshauri Luptan Consult Ltd kwa gharama ya Shilingi Milioni 70.05 na kazi inategemewa kukamilika mwezi Mei, 2022. Kazi za ujenzi zitaanza mara baada ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usanifu wa barabara ya CRDB – Njiapanda ya Kashai yenye urefu wa kilomita 0.5 itaanza mara tu kazi ya usanifu wa kina wa barabara ya Bandarini – Rwamishenye utakapokamilika na fedha za usanifu zitakapopatikana.
MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi Shule ya Sekondari ya Nghoboko kuwa ya kidato cha tano na sita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ili shule ya sekondari iwe na hadhi ya kidato cha tano na sita inatakiwa iwe na vyumba vya madarasa viwili kwa mkondo mmoja, matundu ya vyoo manne, bweni, maktaba, jiko na bwalo la chakula.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Shule ya Sekondari ya Nghoboko bado haijakidhi vigezo vya kuwa ya kidato cha tano na sita. Kwa kutambua umuhimu wa shule hiyo, Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri inaendelea kutafuta fedha kwa ajili kukamilisha miundombinu ya shule hiyo ili iwe na vigezo vya kupandishwa hadhi na kuwa ya kidato cha tano na sita.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA K.n.y. MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa barabara ya kutoka Kata ya Katoma kwenda Nyambaya utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Jimbo la Geita, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Katoma kwenda Nyambaya ina urefu wa kilomita 6.3 ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022 ilianza utekelezaji wa ujenzi wa barabara hii kwa kujenga makalavati manne kwa gharama ya shilingi milioni 22.40 kwa fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Aidha, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali itatenga bajeti ya Shilingi Milioni 67.2 kuendelea na ujenzi wa barabara hiyo kupitia fedha za Mfuko wa Barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga fedha katika bajeti zake za kila mwaka kwa ajili ya matengenezo na ujenzi wa barabara za Wilaya ya Geita ikiwemo barabara ya Katoma hadi Nyambaya kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. DENNIS L. LONDO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara ya kuunganisha Ruaha Mbuyuni, Malolo hadi Uleling’ombe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo, Mbunge wa Mikumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali barabara hii ya Ruaha Mbuyuni - Malolo hadi Uleling’ombe ilikuwa haijaingizwa katika mtandao wa barabara zinazohudumiwa na TARURA. Serikali kupitia TARURA itatenga fedha kiasi cha shilingi milioni 100 katika mpango na bajeti wa mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya usanifu wa awali wa barabara ya Ruaha Mbuyuni, Malolo mpaka Uleling’ombe yenye urefu wa kilometa 27.9. Lengo la usanifu huo ni kupata gharama halisi za ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha changarawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya kupata gharama halisi za usanifu, Serikali kupitia TARURA itaweka katika mipango yake ya bajeti kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Ruaha Mbuyuni, Malolo hadi Uleling’ombe kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupandisha Shule za Sekondari za Mchoteka na Nalasi kuwa za kidato cha tano na kidato cha sita Wilayani Tunduru?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge Jimbo la Tunduru, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili shule ya sekondari iwe na hadhi ya kidato cha tano na sita inatakiwa iwe na vyumba vya madarasa viwili kwa mkondo mmoja, matundu ya vyoo manne, bweni, maktaba/chumba cha kusomea, jiko na bwalo la chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa shule za sekondari Mchoteka na Nalasi bado hazijakidhi vigezo vya kuwa na kidato cha tano na sita. Aidha, kwakutambua umuhimu wa shule hizo, Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha miundombinu ya shule hizo ili ziwe na vigezo vya kupandishwa hadhi na kuwa za Kidato cha Tano na Sita.
MHE. FLORENT L. KYOMBO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakasimu kwa TANROADS Barabara ya Kibaoni, Kakunyu hadi Bugango wakati taratibu za kupandisha hadhi zikiendelea?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Florent Laurent Kyombo, Mbunge wa Jimbo la Nkenge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Kibaoni, Kakunyu hadi Bugango ina sehemu mbili ambazo zinahudumiwa na Wakala mbili za barabara ambazo ni TANROADS na TARURA. Sehemu ya kwanza ya barabara hiyo inaanzia Kibaoni hadi Kakunyu yenye urefu wa kilomita 76 ambayo inahudumiwa na TANROADS na sehemu ya pili inaanzia Kakunyu hadi Bugango yenye urefu wa kilomita 12.4 ambayo inahudumiwa na TARURA.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa mwaka 2022/2023 kupitia TARURA imetenga fedha kiasi cha shilingi milioni 200 kwa ajili ya matengezo ya barabara kutoka Kakunyu hadi Bugango yenye urefu wa kilomita 12.4 kwa kiwango cha changarawe.

Aidha, Serikali itaendelea kuhudumia barabara hiyo na kuhakikisha inapitika wakati wote hadi hapo taratibu za kupandishwa hadhi zitakapokamilika.
MHE. BONNAH L. KAMOLI aliuliza: -

Je, ni lini adha ya Walimu kukaa chini kwa kukosa Ofisi Shule za Msingi za Maendeleo, Bonyokwa na Kinyerezi JICA itatatuliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bonnah Ladislaus Kamoli, Mbunge wa Jimbo la Segerea, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mwongozo wa kuanzishwa kwa shule yoyote ni pamoja na kuwepo kwa jengo la utawala ambalo litawawezesha Walimu kuwa na chumba maalum cha kufanyia maandalizi kabla ya kufundisha (staff room).

Mheshimiwa Spika, Shule za Msingi Maendeleo, Bonyokwa, Kinyerezi JICA na Shule ya Sekondari Kimanga hazina majengo ya utawala ambayo ndio huwa na ofisi ya walimu (staff room) hivyo, baadhi ya madarasa ya ziada yamekuwa yakitumika kama ofisi wakati Serikali ikifanya utaratibu wa kujenga ofisi.

Mhesmiwa Spika, ili kutatua changamoto ya Ofisi za Walimu katika Jiji la Dar es Salaam, Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeielekeza Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya utawala katika shule hizo.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza: -

Je ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Soko, Stendi, Dampo na Machinjio na barabara kilomita 12 za lami kupitia TACTIC katika Mji wa Mbulu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mji wa Mbulu ipo kwenye kundi la tatu lenye miji 18 ambayo utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa stendi kuu ya mabasi, soko jipya na barabara kwa kiwango cha lami unatarajiwa kuanza mwaka huu wa fedha 2022/2023 kwa kuandaa mipango kabambe (master plans).

Mheshimiwa Spika, hivi sasa Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeanza kupokea taarifa za hatua mbalimbali za utambuzi wa mipaka ya kila mji pamoja na taarifa nyingine kwa ajili ya kuandaa hadidu za rejea ili kuwapata Washauri waliobobea katika kuandaa mipango kabambe.

Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilisha maandalizi ya mipango kabambe, kazi ya usanifu kwa halmashauri za kundi hili utaanza mwaka ujao wa fedha 2023/2024 na kazi za ujenzi zinategemea kuanza katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa vibali ili kuajiri walimu na kuondoa upungufu wa walimu uliopo nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutatua na kukabiliana na changamoto ya upungufu wa walimu nchini kwa kutoa vibali vya ajira za walimu ambapo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 iliajiri walimu 14,949 na mwaka wa fedha 2021/2022 iliajiri walimu 9,800.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea na mpango wa kuajiri watumishi wakiwemo walimu ili kukabiliana na upungufu kulingana na mahitaji na upatikanaji wa fedha.
MHE. MARTHA F. MARIKI aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kutatua changamoto ya uhaba wa walimu katika shule za pembezoni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Festo Mariki, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitoa ajira ili kukabiliana na upungufu wa walimu shuleni, unaotokana na walimu kustaafu, kuacha kazi, kufukuzwa, kufariki na ongezeko la idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa. Tangu mwaka 2018/2019 hadi mwaka 2021/2022, Serikali imeajiri jumla ya walimu 26,598 wakiwemo walimu 16,640 wa shule za msingi na walimu 9,958 wa shule za sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina hakikisha walimu wanaajiriwa na kupangwa katika shule zenye uhitaji zaidi, hususan zilizoko maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2020 Ofisi ya Rais – TAMISEMI iliboresha mfumo maalum wa maombi ya ajira na upangaji wa walimu ujulikanao kama Teachers Allocation Protocol. Kupitia mfumo huo, shule zenye upungufu mkubwa wa walimu hususan zilizoko vijijini hubainishwa, ambapo walimu huomba ajira moja kwa moja kwa kuchagua shule husika iliyopo katika mfumo. Aidha, Ofisi ya Rais – TAMISEMI imetoa maelekezo kwa Makatibu Tawala wa Mikoa yote Tanzania Bara kufanya msawazo wa walimu kutoka shule zenye ziada na kuwapeleka katika shule zenye upungufu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuajiri walimu kulingana na mahitaji na upatikanaji wa fedha ili kukabiliana na uhaba wa walimu hususani katika maeneo ya pembezoni.
MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Mbinga Luwaita kupitia Mradi wa Agri-connect kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas William Mbunda Mbunge wa Mbinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Agri-connect ni programu inayofadhiliwa na Jumuiya ya Umoja wa Ulaya ambapo inahusisha ujenzi wa barabara kwa lengo la kusafirisha mazao kutoka shambani au sehemu za uzalishaji kwenda kwenye masoko, viwanda na maghala. Aidha, utekelezaji wa mradi huu utafanyika kwa awamu Tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti barabara ya Luwaita ipo katika Awamu ya Tatu ya programu ya Agri-connect itakayoanza mwaka wa fedha 2023/2024. Kwa sasa, awamu ya tatu ipo kwenye hatua ya uainishaji, uhakiki na upangaji wa vipaumbele vya barabara katika mikoa sita, ambayo ni Iringa, Njombe, Ruvuma, Mbeya, Katavi na Songwe kwa kusimamiwa na Wizara ya kilimo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha za kutosha za ujenzi wa barabara za Wilaya ya Same baada ya kutengewa 9.5% tu ya fedha za TARURA kwa mwaka 2018/2019?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same ina mtandao wa barabara zipatazo kilometa 874.64 ambazo ni sawa na asilimia 18.89 ya mtandao wote wa barabara katika Mkoa wa Kilimanjaro wenye kilometa 4,629.45.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2018/2019 Wilaya ya Same ilitengewa jumla ya shilingi bilioni 1.29 sawa na asilimia 12.81 ya bajeti ya Mkoa wa Kilimanjaro ya shilingi bilioni 10.13. Hata hivyo, bajeti kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya Same imekuwa ikipanda kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Wilaya ya Same ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 3.70 sawa na asilimia 16.24 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 22.83. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 5.80 sawa na asilimia 18.32 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 31.65.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Same kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kuzingatia mtandao wa barabara uliopo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha za kutosha za ujenzi wa barabara za Wilaya ya Same baada ya kutengewa 9.5% tu ya fedha za TARURA kwa mwaka 2018/2019?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same ina mtandao wa barabara zipatazo kilometa 874.64 ambazo ni sawa na asilimia 18.89 ya mtandao wote wa barabara katika Mkoa wa Kilimanjaro wenye kilometa 4,629.45.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2018/2019 Wilaya ya Same ilitengewa jumla ya shilingi bilioni 1.29 sawa na asilimia 12.81 ya bajeti ya Mkoa wa Kilimanjaro ya shilingi bilioni 10.13. Hata hivyo, bajeti kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya Same imekuwa ikipanda kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Wilaya ya Same ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 3.70 sawa na asilimia 16.24 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 22.83. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 5.80 sawa na asilimia 18.32 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 31.65.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Same kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kuzingatia mtandao wa barabara uliopo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha za kutosha za ujenzi wa barabara za Wilaya ya Same baada ya kutengewa 9.5% tu ya fedha za TARURA kwa mwaka 2018/2019?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same ina mtandao wa barabara zipatazo kilometa 874.64 ambazo ni sawa na asilimia 18.89 ya mtandao wote wa barabara katika Mkoa wa Kilimanjaro wenye kilometa 4,629.45.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2018/2019 Wilaya ya Same ilitengewa jumla ya shilingi bilioni 1.29 sawa na asilimia 12.81 ya bajeti ya Mkoa wa Kilimanjaro ya shilingi bilioni 10.13. Hata hivyo, bajeti kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya Same imekuwa ikipanda kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Wilaya ya Same ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 3.70 sawa na asilimia 16.24 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 22.83. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 5.80 sawa na asilimia 18.32 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 31.65.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Same kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kuzingatia mtandao wa barabara uliopo.
MHE. DEUS C. SANGU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga walau KM Tatu za barabara ya lami katika Mji wa Laela - Sumbawanga ambao hauna barabara ya lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deus Clement Sangu Mbunge wa Jimbo la Kwela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa Ujenzi wa barabara za lami katika Mji mdogo wa Laela ambazo zitachochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa Wananchi wa Mji huo. Aidha, katika Mwaka wa Fedha 2022/ 2023 Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini inatarajia kufanya zoezi la kuainisha na kuzifanyia usanifu barabara zenye urefu wa kilomita Tatu kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hizo ili kupata gharama halisi za ujenzi.

Mheshimiwa Spika, baada ya utambuzi na usanifu wa barabara hizo kukamilika, TARURA itaweka katika vipaumbele vyake barabara hizo kwa ajili ya kuanza ujenzi katika bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024.
MHE. FRANCIS I. MTINGA aliuliza: -

Je, Serikali inatumia vigezo gani katika mgawanyo wa Watumishi wapya kwenye Halmashauri hususani walimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Isack Mtinga Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikiajiri watumishi hususani Walimu kulingana na bajeti iliyotengwa kwa mwaka husika. Baada ya kuajiri walimu hugawanywa kila Halmashauri kwa kuzingatia idadi ya mikondo, kila shule kuwa na Walimu wasiopungua Nane na Uwiano wa Mwanafunzi kwa Mwalimu (Pupil Teacher Ratio) kwa shule za Msingi.

Mheshimiwa Spika, kwa shule za sekondari vigezo vinavyotumika kugawa Walimu ni kubainisha idadi ya wanafunzi wanaosoma somo kwa kila kidato, kukokotoa idadi ya mikondo ya madarasa ya wanafunzi kwa kila kidato (mkondo mmoja kuwa na wanafunzi 40 kuanzia Kidato cha Kwanza hadi cha Nne na wanafunzi 35 kwa Kidato cha Tano na Sita. Kubainisha idadi ya vipindi vinavyotakiwa kufundishwa kwa kila somo kwa kuzingatia maelekezo ya mtaala na ukomo wa vipindi anavyofundisha Mwalimu kwa kila somo. Kadirio la juu mwalimu anatakiwa kufundisha vipindi vya dakika 40, thelathini na kadirio la chini visipungue ishirini na nne.
MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa daraja la juu Mto Semu katika Kijiji cha Mwamanongu Meatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya Mbunge wa Jimbo la Meatu, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa fedha 2005/ 2006, Serikali kupitia Mfuko wa Barabara ilijenga daraja la chini (drifting) lenye urefu wa mita 100 kwa gharama ya Shilingi Milioni 105 ili kurahisisha mawasiliano katika Kijiji cha Mwamanongu.

Mheshimiwa Spika, TARURA inaendelea na upembuzi yakinifu (Geotechnical Investigation) kwa ajili ya kuanza kazi ya usanifu ili kupata gharama za ujenzi wa daraja la juu katika Mto Semu lililopo katika Kijiji cha Mwamanongu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika kwa usanifu wa Daraja hili, Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa hili daraja.
MHE. RASHID A. SHANGAZI K.n.y. MHE. KENETH E. NOLLO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga daraja la kudumu kwenye Mto Mzizima ili barabara ya Kigwe hadi Chipanga Wilayani Bahi iweze kupitika mwaka mzima?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kenneth Nollo, Mbunge wa Bahi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia TARURA Wilaya ya Bahi, imetenga fedha kiasi cha shilingi milioni 620.23 kwa ajili ya ujenzi wa daraja (box culvert) lenye urefu wa mita 34. Ujenzi wa daraja hili umeanza tarehe 20 Februari, 2022 na unatarajiwa kukamilika tarehe 19 Agosti, 2022 na ujenzi wa mradi huu umefikia asilimia 30. Kazi hiyo inafanywa na Mkandarasi Ravji Construction Ltd.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa ujenzi wa daraja hilo utaifanya barabara ya Kigwe – Chipanga kupitika wakati wote na hivyo kuondoa kero ya wananchi kutumia muda mwingi wa kusubiria maji ya mto yapungue ili wavuke na kuendelea na shughuli za kiuchumi na kijamii.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Je, kwa nini Serikali isipitishe mkakati maalum kwenye bajeti ya mwaka 2022/2023 wa kujenga shule za msingi kwenye vitongoji vyote vyenye watoto zaidi ya 200?

NAIBU WAZIRI, OFISI RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo ya Serikali ni kuwa na Shule ya Msingi kila Kijiji ikiwemo na vitongoji katika jimbo la Sikonge.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ukweli kuwa Jimbo la Sikonge kwa sasa halina shule za msingi za kutosha, Halmashauri ya Sikonge kupitia fedha toka Serikalini na kwa kutumia vyanzo mbalimbali vya mapato vya Halmashauri inaendelea kuhimiza wananchi, jamii na wadau wa maendeleo kujenga miundombinu ya shule za msingi ili kukidhi mahitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kutenga fedha kwa ajili ya kujenga shule za msingi kila kitongoji kutategemeana na hali ya uchumi wa nchi na upatikanaji wa fedha. Hata hivyo, kwa jinsi sera ilivyo hatujafikia hatua ya kujenga shule kwa kila kitongoji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa shughuli ya ujenzi wa shule inawahusisha wananchi na jamii kwa ujumla, napenda kumshauri Mheshimiwa Mbunge kuendelea kushirikiana na wananchi na Halmashauri kujenga shule katika kila kijiji ili kuwezesha wanafunzi wote wenye umri wa kwenda shule kuweza kupata nafasi.
MHE. CHARLES M. KAJEGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza kukarabati Shule za Msingi za Nansimo, Kenkombyo, Kitengule na Namibu zilizopo katika Jimbo la Mwibara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Charles Muguta Kajege Mbunge wa Jimbo la Mwibara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Shule 2,147 shule za msingi kongwe nchini ambazo zilianzishwa kabla ya kupata Uhuru mwaka 1961. Hali ya miundombinu ya shule hizo ni mseto zikiwemo zenye hali nzuri na nyingine zenye miundombinu chakavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais-TAMISEMI imeanza kufanya tathimini ya hali ya miundombinu ya shule zote za msingi kupitia mradi wa BOOST ili kubaini mahitaji ya ujenzi wa miundombinu mipya ya shule na hali ya uchakavu wa miundombinu iliyopo. Tathimini hiyo imeanza mwezi Aprili, 2022 na itakamilika mwezi Julai, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo ya tathimini hiyo yatatumika kuandaa mpango wa uendelezaji na ukarabati wa miundomibinu ya Shule za Msingi kwa miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi mwaka 2025/2026 zikiwemo Shule za Msingi Nansimo, Kenkombyo, Kitengule na Namibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kufanya ukarabati wa miundombinu ya shule kongwe za msingi kadri fedha zitakapopatikana.
MHE. BONNAH L. KAMOLI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa vitendo kwa kuhakikisha inajenga nyumba za Walimu kama inavyofanya kwa Majeshi ya Ulinzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bonnah Ladislaus Kamoli, Mbunge wa Segerea kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya mahitaji ya Nyumba za Walimu Nchini.

Mheshimiwa Spika, ili kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa vitendo, Serikali itaendelea kupeleka fedha kwa ajili ya kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji ikiwemo ujenzi wa nyumba za walimu kulingana na upatikanaji wa fedha kupitia vyanzo mbali mbali.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi bilioni 37.85 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu katika shule za Sekondari na shilingi bilioni
43.63 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu katika Shule za Msingi.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutoa fedha kwa ajili ya nyumba za walimu katika maeneo ambayo kunauhitaji mkubwa likiwemo na jimbo la Segerea kadri fedha zitakavyopatikana.
MHE. FLORENT L. KYOMBO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaitengea bajeti barabara inayounganisha Uganda na Tanzania ya Kibaoni - Kakunyu kwenda Bugango mpakani ambayo iko chini ya TARURA wakati taratibu za kupandishwa hadhi zikiendelea ili iweze kupitika wakati wote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Florent Laurent Kyombo, Mbunge wa Nkenge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hiyo ya Kakunyu - Bugango ni muhimu kwa kuwa inaungaisha Nchi jirani ya Uganda pia hutumika katika kukuza shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa Missenyi.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu huo, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), kwa mwaka wa fedha 2021/2022 ilitenga jumla ya Shilingi Million 41.08 kwa ajili ya matengenezo ya barabara hiyo katika maeneo korofi yenye urefu wa kilomita 3.0 na kazi hiyo imefanyika na kukamilika.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali imeendelea kuona umuhimu wa kuhakikisha kuwa wananchi wa Missenyi wanaweza kufika katika mpaka wa Bugango kwa kutenga jumla ya Shilingi Milioni 34.92 katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya matengenezo ya barabara nyingine iliyopo jirani iitwayo Missenyi Ranchi - Bugango jumla ya kilomita 17.3 ambapo Mkandarasi yupo eneo la kazi anaendelea ukamilishaji wa matengenezo hayo. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya kujenga vyumba vinne vya madarasa na bweni katika Shule ya Sekondari Matombo Kata ya Konde?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule ya Sekondari Matombo iko katika Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro. Shule hii ni ya kidato cha kwanza hadi cha sita, hivyo, kutokana na ongezeko la wanafunzi wanaofaulu mtihani darasa la saba na kidato cha nne kila mwaka shule inahitaji miundombinu ya kutosha ikiwemo bweni na madarasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI alitembelea na kuona hali halisi ya miundombinu ya Shule ya Sekondari Matombo tarehe 22 Septemba, 2021 na kuahidi kujenga madarasa manne na bweni moja mwaka wa fedha 2022/2023 kupitia programu zake mbalimbali ikiwemo SEQUIP na EP4R zinazojenga miundombinu ya elimu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.
MHE. JOHN M. SALLU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga daraja la Kwasunga – Handeni Vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa John Marko Sallu Mbunge wa Jimbo la Handeni Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Handeni na Wilaya ya Bagamoyo inatenganishwa na Mto Mligazi. Mto huu umekuwa changamoto kubwa kwa watumiaji wa barabara ya Kwasunga inayotoka Mkata kuelekea Kwasunga kuunganisha vijijni vya Miyono katika Wilaya ya Bagamoyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2021/2022 TARURA Mkoa wa Tanga imeingia mkataba Na. AE/092/2021-2022/TAG/C/01 na Mkandarasi Mshauri kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kupitia Kampuni ya BICO wenye gharama ya Shilingi milioni 42.98 kwa ajili ya uchunguzi wa miamba. Kazi ya uchunguzi imeshafanyika na kwa sasa mkandarasi huyo yupo katika hatua ya mwisho ya kuwasilisha taarifa ya matokeo ya uchunguzi ambapo baada ya kazi ya usanifu wa daraja pamoja na uandaaji wa michoro na gharama za ujenzi Serikali itatenga fedha za ujenzi wa daraja hilo.
MHE ASIA A. HALAMGA K.n.y. MHE. EDWARD O. KISAU aliuliza: -

Je, ni nini kauli ya Serikali juu ya kusajili na kuboresha miundombinu ya Shule Shikizi zilizojengwa kwa nguvu za Wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edward Kisau Olelekaita, Mbunge wa Jimbo la Kiteto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo shikizi ni vituo vilivyojengwa kwenye maeneo ambayo hayana shule au shule ziko umbali mrefu kutoka kwenye maeneo wanayoishi wananchi. Vituo hivi kabla ya kusajiliwa kuwa shule kamili hufanyiwa ukaguzi na ufuatiliaji na Wathibiti Ubora wa Shule kwa kushirikiana na Maafisa kutoka ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri. Kama hakuna mapungufu taarifa ya ukaguzi pamoja na barua ya kuomba usajili hutumwa kwa Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili Shule husika ipate usajili.

Mheshimiwa Spika, ili vituo shikizi viweze kusajiliwa na kuwa shule halmashauri pamoja na wananchi wa vijiji husika wayafanyie kazi maelekezo ya wathibiti ubora wa shule ili shule hizo ziweze kupata usajili.
MHE. IDDI K. IDDI aliuliza: -

Je, Serikali inaichukulia hatua gani TARURA Msalala kwa kuchelewesha mikataba na kuwapa kazi wakandarasi wasio na uwezo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Jimbo la Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022, jumla ya mikataba 11 inatekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Msalala yenye jumla ya Shilingi bilioni 2.66. Kati ya Mikataba hiyo 11 Mikataba minane ilisainiwa mwezi Agosti, 2021 na Novemba, 2021 ambayo yote inatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2022.

Mheshimiwa Spika, mikataba mitatu haikufikia hatua ya kusainiwa kutokana na kutopatikana kwa Makandarasi kwa wakati baada ya kushindwa kukidhi vigezo vilivyowekwa kwenye zabuni. Hivyo, Mikataba hiyo mitatu imesainiwa mwezi Februari na Machi, 2022 baada ya kuwapata Makandarasi waliopata zabuni.

Mheshimiwa Spika, kutokana maelezo hayo, Makandarasi wanaotekeleza mikataba minane imesainiwa kwa wakati kwa mujibu wa taratibu za ununuzi na mikataba mitatu ilichelewa kusainiwa kutokana na kushindwa kupatikana Makandarasi na zabuni kutangazwa upya.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA K.n.y. MHE. SALMA R. KIKWETE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati mkubwa katika Shule ya Msingi Kingurungundwa iliyopo Mchinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsate sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete, Mbunge wa Mchinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuna shule za msingi kongwe 2,147 nchini ambazo zilianzishwa kabla ya kupata Uhuru mwaka 1961. Hali ya miundombinu ya shule hizo ni mseto zikiwemo zenye hali nzuri na nyingine zenye miundombinu chakavu.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI imeanza kufanya tathimini ya hali ya miundombinu ya shule zote za msingi kupitia mradi wa BOOST ili kubaini mahitaji ya ujenzi wa miundombinu mipya ya shule na hali ya uchakavu wa miundombinu iliyopo. Tathimini hiyo imeanza mwezi Aprili, 2022 na itakamilika mwezi Julai, 2022.

Mheshimiwa Spika, matokeo ya tathimini hiyo yatatumika kuandaa mpango wa uendelezaji na ukarabati wa miundomibinu ya shule za msingi kwa miaka mitano, kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi mwaka 2025/2026 ikiwemo Shule ya Msingi Kingurungundwa.
MHE. FRANCIS L. MTEGA aliuliza: -

Je, lini Serikali italigawa Jimbo la Mbarali na kuwa na Halmashauri mbili ili kusogeza huduma karibu na wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis leonard Mtega Mbunge wa Jimbo la Mbarali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, halmashauri huanzishwa kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa, Sura ya 287 na 288 pamoja na Mwongozo wa Uanzishwaji wa Maeneo ya Utawala wa Mwaka 2014. Mwongozo huo umeainisha vigezo na taratibu zinazopaswa kufuatwa ili kuanzisha Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria hii, hatua ya awali inahusisha kupata ridhaa ya vijiji, Kamati za Maendeleo za Kata, Baraza la Madiwani la Halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC). Baada ya hatua hii, maombi hayo yanawasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya uhakiki na tathmini na kuwasilishwa kwa mamlaka husika ili itoe uamuzi.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais TAMISEMI haijapokea maombi ya kuigawa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali. Hivyo, nashauri taratibu za uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala zifuatwe.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya katika Kata ya Mangopacha Nne ili kuwanusuru Akina Mama na tatizo la ukosefu wa huduma wakati wa kujifungua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anastazia James Wambura, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetoa fedha Shilingi bilioni 86 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya 234 kwenye kata za kimkakati kote nchini. Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara imepokea Shilingi milioni 250 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Kituo cha Afya Mkunwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga vituo vya kutolea huduma za afya kwenye kata za kimkakati zenye uhitaji mkubwa ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kituo cha afya kwenye Kata ya Mango Pacha Nne.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani kudhibiti magari yanayopakua na kupakia mizigo katika maeneo ya Kariakoo, Mtaa wa Msimbazi na Barabara ya Morogoro ili kupunguza kero kwa wakazi wa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kudhibiti magari makubwa yanayopakia na kupakua mizigo katika maeneo ya Kariakoo, Mtaa wa Msimbazi na barabara ya Morogoro, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imeweka utaratibu wa kudhibiti magari hayo kwa kutoa vibali Maalum vinavyowaruhusu kuingia mjini kama ilivyotamkwa kwenye kifungu cha 8 cha Sheria Ndogo za Matumizi ya Barabara za Halmashauri ya Manispaa ya Ilala (ambayo ndiyo Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwa sasa) za mwaka 2015.

Mheshimiwa Spika, mtu yeyote atakayeingiza lori au kontena bila kibali atakuwa ametenda kosa, na akipatikana na hatia atatozwa faini isiyopungua Shilingi elfu hamsini hadi laki tatu kulingana na uzito wa gari, au kifungo kisichozidi miezi 12 jela, au vyote kwa pamoja. Hata hivyo, halmashauri kwa kushirikiana na vyombo vingine, ina utaratibu wa kutoa elimu kwa madereva, wamiliki wa magari makubwa na kwa umma ili kuwapa uelewa wa athari zinazotokana na uingizaji wa magari makubwa kiholela.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ina mpango wa kujenga maegesho ya kisasa katika eneo la Mnazi Mmoja kwa ajili ya magari mbalimbali yakiwemo magari ya mizigo.
MHE. AGNES M. MARWA aliuliza: -

Je, ni vikundi vingapi vya wanawake na vijana vimewezeshwa kufanya uvuvi wa vizimba Ziwa Victoria?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kabla sijajibu swali, naomba kwa kifupi sana nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuniamini na kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Rais ameweka mtu sahihi, mahali sahihi na kazi itafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Mathew Marwa, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2021/2022, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Nyegezi Mwanza ilitoa mafunzo ya ufugaji samaki kwa vizimba kwa vijana 288 (wanaume 208 na wanawake 80). Vijana hao walitoka katika Wilaya za Nyamagana – 74; Ilemela – 54; Magu – 31; Misungwi – 21; Ukewere – 51; Sengerema - 28 na Buchosa - 29.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2022/2023, Serikali imetenga shilingi bilioni 20 kwa ajili ya kuwawezesha wakuzaji viumbe maji nchini. Kati ya fedha hizo shilingi bilioni 15.1 zitatolewa kwa wafugaji samaki kwa vizimba katika Ziwa Victoria kama mikopo ya pembejeo kwa masharti nafuu kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB). Jumla ya wananchi 3,154 wanatarajiwa kunufaika kwa kupata mikopo ya vizimba, vifaranga na chakula cha samaki. Kati ya hao vijana ni 241, wanawake 290 na kampuni mbili za wanawake. Ahsante sana.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza: -

Je, ni kwa nini Serikali haijagawa fedha kwa ajili ya ufugaji wa vizimba vya samaki katika Ziwa Nyasa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Ruvuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ili kufuga samaki kwa vizimba inabidi kuainisha maeneo yanayofaa ziwani kwa kuzingatia vigezo vya kisheria na kitaalam. Katika awamu ya kwanza Serikali ilitoa fedha katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa Victoria ambayo ilishakidhi vigezo vya kisheria na kitaalam baada ya kufanyiwa tathmini katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 na 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2023/2024, Serikali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi (TAFIRI) imepanga kufanya tathmini ya kimkakati ya mazingira (Strategic Environmental Assessment) katika Ziwa Nyasa ili kuanisha maeneo yanayofaa kwa ufugaji wa samaki kwa vizimba kwa kuzingatia vigezo vya kisheria na kitaalam. Pia (TAFIRI) itaanza ufugaji samaki kwa majaribio kwa kushirikiana na wananchi kufanya uzalishaji wa vifaranga vya samaki aina ya magege (Oreochromis karongae) na ufugaji wake kwa vizimba. Hatua hii inalenga kuwajengea uwezo wananchi ili waweze kuendelea na ufugaji pindi taratibu zitakapokamilika.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaweka katazo la kisheria la kuswaga mifugo ili kuzuia uharibifu wa mazingira?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, usafirishaji wa mifugo hufanyika chini ya Sheria ya Magonjwa ya Wanyama, Sura 156 na Kanuni zake za Udhibiti wa Usafirishaji wa Wanyama na Mazao ya Wanyama, G.N. 28 za mwaka 2007, ambapo usafirishaji wa mifugo kutoka wilaya moja kwenda nyingine hufanyika baada ya mifugo kukaguliwa na wataalam na kupatiwa kibali cha kusafirishwa. Aidha, Waraka wa Rais Na.1 wa Mwaka 2002 uliziagiza Serikali za Mitaa kote nchini kutunga sheria ndogo ili kuzuia uswagaji wa mifugo.

Mheshimiwa Spika, kwa maelezo hayo hapo juu inathibitisha kwamba sheria ipo. Hivyo basi, wafugaji wanahimizwa kuzingatia Sheria ya Magonjwa ya Wanyama, Sura 156 pamoja na sheria ndogo zilizopo ndani ya halmashauri zao zinazozuia uswagaji wa mifugo. Pia, nitumie fursa hii kuzielekeza halmashauri ambazo mpaka sasa hazijatunga sheria ndogo za kuzuia uswagaji wa mifugo zifanye hivyo mara moja.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha Ludewa kwa ajili ya Miradi ya Ufugaji Samaki kwenye vizimba ndani ya Ziwa Nyasa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ufugaji wa samaki kwa vizimba ziwani unafanyika katika maeneo yaliyokidhi vigezo vya kisheria na kitaalam. Serikali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) hufanya tathmini ya kimkakati ya mazingira (Strategic Environmental Assessment) ili kuhakikisha maeneo husika yanakidhi vigezo kabla ya kuanza uwekezaji. Tathmini hii imepangwa kufanyika kwa awamu katika Maziwa yetu yote na kwa mwaka 2021/2022 na 2022/2023 ilianza katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka 2023/2024, Serikali imepanga kuendelea kufanya tathmini katika Ziwa Nyasa ikiwemo Ludewa ili kutambua maeneo yanayofaa kwa ufugaji samaki katika vizimba. Pia, Serikali itawezesha TAFIRI kufanya majaribio ya ufugaji samaki kwa kushirikiana na wananchi utakaojumuisha uzalishaji wa vifaranga vya samaki aina ya magege (Oreochromis karongae) na ufugaji wake kwa vizimba. Hatua hii inalenga kuwajengea uwezo wananchi wa ufugaji wa samaki pindi tathmini itakapokamilika. Vile vile, hatua hii itawawazesha wananchi wa Ludewa na Ziwa Nyasa kwa ujumla kunufaika na fursa za mikopo zilizopo kwa ajili ya kuwezesha ufugaji samaki kwa vizimba. Ahsante.
MHE. VINCENT P. MBOGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga malambo ya kunyweshea mifugo katika Kata ya Chala, Kate, Myula na Nkandasi Wilayani Nkasi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vincent Paul Mbogo, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto ya upungufu wa maji kwa ajili ya mifugo katika Kata za Chala, Kate, Myula na Nkandasi, Serikali katika mwaka wa fedha 2023/2024, imepanga kufanya tathmini ya miundombinu ya maji na usanifu utakaowezesha kujenga malambo au kuchimba visima virefu katika maeneo hayo. Matokeo ya tathmini hiyo yataiwezesha Serikali kujenga miundombinu hiyo kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kuongezeka kwa changamoto ya uhaba wa maji kwa ajili ya mifugo, nazikumbusha Halmashauri za Wilaya nchini kutekeleza Waraka wa Rais Na.1 wa mwaka 2002 kuhusu kutenga asilimia 15 ya mapato yatokanayo na Sekta ya Mifugo ili kujenga na kukarabati miundombinu ya maji. Pia, nitoe wito kwa wafugaji na wadau wengine kuwekeza kwenye ujenzi wa malambo au kuchimbaji visima virefu.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA K.n.y. MHE. ALLY M. KASSINGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Soko la Samaki Kilwa Kivinje?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imefanya tathmini ya athari za mazingira na kijamii katika eneo la Kitongoji cha Miramba kilichopo Kilwa Kivinje kwa ajili ya kujenga miundombinu ya kuhifadhia mazao ya uvuvi ya chumba cha ubaridi, vichanja vya kukaushia dagaa na kuweka mtambo wa kuzalisha barafu na wa kukaushia dagaa kwa kutumia umeme.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi inayofadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa wa Kuendeleza Kilimo (IFAD) itaweka miundombinu hiyo katika eneo hilo. Aidha, Serikali itaendelea na mpango wa kufanya tathmini ya athari ya mazingira na kijamii kwa ajili ya ujenzi wa soko la samaki katika eneo hilo kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH aliuliza: -

Je, kuna mikakati gani ya kudhibiti mifugo katika Bonde la Ihefu na Mto Kilombero?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Soud Mohammed Jumah, Mbunge wa Jimbo la Donge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Oktoba, 2022 Serikali kupitia Kamati ya Mawaziri Nane wa Kisekta inayoshughulikia migogoro ya ardhi katika vijiji 975 nchini, ilitoa tamko kuhusu utatuzi wa mgogoro wa mpaka kati ya Hifadhi ya Taifa Ruaha na baadhi ya vijiji vya Wilaya za Mbarali na Chunya. Ili kudhibiti mifugo katika Bonde la Ihefu na Mto Kilombero, jumla ya vijiji 16 vimeandaa mipango ya matumizi ya ardhi ya vijiji na kutenga maeneo kwa ajili ya malisho ili kuwezesha ufugaji katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kudhibiti mifugo kutoka katika maeneo mengine kwenda kwenye Bonde la Mto Kilombero kutafuta malisho na maji katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali inajenga mabwawa ya maji kwa ajili ya mifugo katika Halmashauri za Morogoro DC Kijiji cha Kongwa na Kibaha DC Kijiji cha Viyenze. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imeanzisha mashamba darasa 100 ya malisho katika Halmashauri 44 zikiwemo Halmashauri zinazopakana na Bonde la Ihefu na Mto Kilombero ili wafugaji waweze kujifunza kuzalisha malisho na hivyo kutulia katika maeneo yao ya ufugaji.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha Wavuvi ambao wameunda vikundi na kuanza ufugaji wa vizimba katika Jimbo la Busanda?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bryceson Magessa Tumaini, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2022/2023, Wizara kwa kushirikiana na Benki ya Maendelo ya Kilimo (TADB) inatekeleza mradi wa kutoa mikopo yenye masharti nafuu na isiyo na riba ya pembejeo za ufugaji samaki ikijumuisha vizimba, vifaranga vya samaki na chakula cha samaki kwa ajili ya ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba. Aidha, jumla ya wanufaika 3,154 wameainishwa kunufaika na mradi huo ikijumuishwa vikundi 93, kampuni 10, na watu binafsi 32. Kwa upande wa Geita DC vikundi vitatu vinatarajiwa kunufaika na program hiyo ikiwemo kikundi cha Tumaini chenye wanachama 10 kutoka Jimbo la Busanda. Vikundi hivi vitapatiwa mikopo ya pembejeo za ufugaji samaki kwenye vizimba yenye thamani ya Shilingi milioni 69.4 kwa kila kikundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali itaendelea kutekeleza mradi wa kutoa mikopo yenye masharti nafuu na isiyo na riba ya pembejeo za ufugaji samaki kwa kuwawezesha wafugaji samaki wenye vizimba 893. Hivyo, natoa wito kwa wafugaji samaki nchini wakiwemo wale wa Jimbo la Busanda kuendelea kuchangamkia fursa hii kwa kujiunga katika vikundi na kuanzisha vyama vya ushirika wa ufugaji samaki.
MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia Wavuvi wa Ziwa Tanganyika zana za uvuvi za kisasa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto za wavuvi zilizopo ikiwemo ukosefu wa zana za kisasa za uvuvi. Katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga fedha kwenye programu maalum ya mikopo wenye masharti nafuu kutoka Shirika la Fedha Duniani (IMF) kupitia dirisha la extended credit facilities (ECF) kwa ajili ya kuwawezesha wavuvi boti za kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza mpango huo, Serikali inakamilisha taratibu za kutoa boti 158 kwa mkopo kupitia Benki ya Kilimo (TADB) kwa Vyama vya Ushirika 45, Vikundi vya Wavuvi 71 na watu binafsi 43. Aidha, katika Ukanda wa Ziwa Tanganyika jumla ya Vyama vya Ushirika vinne, Vikundi vinne na watu binafsi watano wanatarajiwa kunufaika na mikopo wa boti hizo usiokuwa na riba.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali kupitia TADB inatoa mitaji kwa wakulima, wafugaji na wavuvi ili kuboresha shughuli zao za maendeleo. Aidha, Serikali inawahimiza wavuvi kujiunga katika vikundi na kuanzisha vyama vya ushirika vya msingi, SACCOS na VICOBA ili waweze kukopesheka na kuweza kununua zana na vyombo bora vya uvuvi.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA K.n.y. MHE. ASYA SHARIF OMAR aliuliza:-

Je, kuna mkakati gani wa kutoa mafunzo ya kuogelea kwa wakulima wa Mwani Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asya Sharif Omar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa zao la mwani katika kuongeza kipato, ajira na kukuza uchumi katika ukanda wa pwani na Taifa kwa ujumla. Vilevile, inatambua kuwa, zaidi ya asilimia 90 ya wakulima wa mwani ni wanawake. Ili kuwa na kilimo endelevu na kulinda usalama wa wakulima wa mwani wawapo katika shughuli zao, ni muhimu wakulima hawa kuwa na ujuzi wa kuogelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimekuwa na mikakati mbalimbali kuhakikisha wakulima wa mwani wanapatiwa nyenzo bora za kuhakikisha usalama mahali pa kazi. Katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zitatoa mafunzo ya kuogelea kwa wakulima wa mwani pamoja na kununua na kusambaza vifaa vya kulinda usalama wakiwa kwenye maji wakishughulika na kilimo cha mwani.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL aliuliza

Je, lini Serikali itafanya ukarabati wa mnada wa ng'ombe na mbuzi wa Olokii?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya kufanya biashara ya mifugo hapa nchini kwa kujenga na kukarabati minada ya mifugo ya awali, minada ya upili na minada ya mipakani. Kwa sasa kuna jumla ya minada 504 ya awali, 17 ya upili na 12 ya mpakani. Mnada wa Olokii (Themi) ni moja ya minada ya upili ambao upo chini ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 na Mwaka wa Fedha 2022/2023, Serikali imejenga na kukarabati minada 12 katika maeneo mbalimbali nchini. Katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali itafanya usanifu wa miundombinu ya mnada wa Olokii (Themi) ili uweze kuingizwa katika Mpango wa Bajeti wa mwaka wa fedha 2024/2025 kwa ajili ya kufanyiwa ukarabati.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakuja na mpango wa ujenzi wa vizimba vya ufugaji wa samaki katika Ziwa Duluti?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvivu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ziwa Duluti ni sehemu ya Hifadhi ya Msitu wa Asili wa Ziwa Duluti ambao unasimamiwa na Wakala ya Huduma za Misitu (TFS). Hifadhi hiyo ni kivutio cha utalii wa ikolojia, picha, kutembea msituni, kuangalia ndege na viumbe wengine, boti za kupiga kasia na uvuvi wa burudani. Kutokana na hadhi ya eneo tajwa, shughuli za kiuchumi zinadhibitiwa ili kutokuharibu ikolojia na bioanuwai iliyopo katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumuahidi Mheshimiwa John Danielson Pallangyo Mbunge, kuwa katika mwaka wa fedha 2023/2024 Wizara yangu itafanya utafiti kupitia Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi TAFIRI kwa kushirikiana na TFS ili kuona kama ufugaji wa Samaki wa vizimba unaweza kufanyika bila kuathiri ikolojia na bioanuai katika Ziwa Duluti.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamalizia fedha za ujenzi wa Soko la samaki Bagamoyo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu : -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo n Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Muharami Shabani Mkenge, Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Soko la Samaki Bagamoyo limejengwa kwa fedha za Serikali kupitia Halmashauri ya Bagamoyo na limeshaanza kutumiwa na wadau wa uvuvi. Kwa sasa soko hili lina miundombinu ya jengo la mnada, jengo la kuhifadhia samaki, jengo la maliwato, jengo la kuhifadhia taka, kibanda cha askari/mlinzi na jengo la kukaangia samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukamilisha soko hili kuendana na michoro iliyopo, inahitajika kuongezewa jengo moja la kukaangia samaki, jengo la mama lishe, jengo la maduka na jengo la ofisi. Aidha, katika mwaka 2024/2025, Serikali imepanga kujenga miundombinu hiyo iliyosalia katika soko hilo kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (Agriculture and Fisheries Development Programme - AFDP).

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, katika mwaka 2023/2024, Serikali kupitia programu ya kuendeleza kilimo na uvuvi itaweka vichanja kumi (10) vya kuanikia dagaa, mahema mawili (2) ya kukaushia samaki kwa kutumia nguvu ya jua na mtambo mmoja wa kuzalisha barafu katika eneo la karibu na soko hilo.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza: -

Je, ni utaratibu gani umewekwa wa kuwapatia mikopo wavuvi wadogo wa upande wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua mahitaji makubwa ya mikopo kwa wavuvi, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinakamilisha maandalizi ya mradi wa uchumi wa buluu (Tanzania Scaling Up Sustainable Fisheries and Acquaculture Management Project – TASFAM) utakaotekelezwa Tanzania Bara na Zanzibar. Mradi huu unafadhiliwa na Benki ya Dunia (World Bank) na utawawezesha wavuvi wa Tanzania Bara na Zanzibar kupata mikopo ya masharti nafuu kupitia taasisi za kifedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, katika juhudi za kusaidia wavuvi wadogo, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Uvuvi Bahari Kuu (DSFA) ina programu za kuwawezesha wavuvi wadogo upande wa Zanzibar kwa kuwapatia mafunzo ya uvuvi wa kisasa pamoja na fursa za upatikanaji wa mikopo ya zana bora za uvuvi kutoka Taasisi mbalimbali za kibenki ikiwemo Benki ya Kilimo Tanzania (TADB).
MHE. JUMA USONGE HAMAD aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuzitangaza ndani na nje ya nchi bidhaa zinazotokana na Zao la Mwani?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Usonge Hamad Juma, Mbunge wa Jimbo la Chaani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitangaza bidhaa za zao la mwani nchini kupitia maonyesho, warsha na matamasha mbalimbali ikiweno Sherehe za Wakulima Nane Nane, Maonesho ya Biashara za Kimataifa Saba Saba, Sherehe za Siku ya Mvuvi Duniani na Siku ya Chakula Duniani. Pia bidhaa za mwani zinatangazwa katika vyombo vya habari mbalimbali ikiwemo runinga, redio, magazeti na mitandao ya kijamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Korea Kusini imeandaa Tamasha la Uvuvi Korea na Afrika (Korea African Fisheries Forum) litakalofanyika Zanzibar kuanzia tarehe 14 hadi 15 Juni, 2023 litakalojumuisha wadau kutoka Korea Kusini na Senegal. Tamasha hili linalenga kutangaza shughuli za uvuvi na ukuzaji viumbe maji za Afrika ikiwemo zao la mwani na bidhaa zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Serikali inaandaa mpango wa kutangaza bidhaa za mwani nje ya nchi kwa kutumia Balozi zetu zilizopo katika nchi mbalimbali kupitia matamasha, vikao na warsha zitakazofanyika katika nchi hizo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya kampuni zilizo chini ya NARCO ili kuona tija zake katika uchumi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) inamiliki ranchi 15 na imewekeza katika ranchi nane kati ya hizo. Aidha, NARCO imegawa vitalu na kukodishwa kwa wafugaji na kampuni binafsi kwa ajili ya ufugaji wa kisasa na wa kibiashara. Mwezi Oktoba, 2022 Serikali kupitia Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) ilifanya tathmini kwenye vitalu 116 ambavyo vimekodishwa kwa wafugaji ili kubaini hali ya uwekezaji kulingana na mipango ya biashara iliopo kwenye mikataba yao. Katika tathmini hiyo ilibainika kuwa wawekezaji 76 wamewekeza kulingana na mkataba na wawekezaji 40 wameonesha kutofanya vizuri kulingana na mikataba yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tathimini ilibaini kuwa NARCO inakabiliwa na changamoto za kimtaji, hivyo imeandaa andiko la mabadiliko ili kuiwezesha kupata mtaji kutoka vyanzo mbalimbali vya fedha. Hata hivyo, ili kuimarisha Kampuni ya NARCO na kuongeza tija, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imewekeza kiasi cha shilingi bilioni 4.6 kwa ajili ya kununua ng’ombe wazazi, kuchimba visima virefu na kununua mitambo ya kulima, kuvuna na kuhifadhi malisho ya mifugo.
MHE. MIRAJI J. MTATURU K.n.y. MHE. ALLY J. MAKOA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga majosho katika Kata za Kolo, Kingale na Bolisa?

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Ally Juma Makoa, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na mpango wa ujenzi wa majosho nchini ili kudhibiti magonjwa yanayoenezwa na kupe. Katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Sekta ya Mifugo, imetenga jumla ya shilingi bilioni 5.7 kwa ajili ya ujenzi wa majosho 246 katika Halmashauri 63 nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Kondoa Mjini jumla ya shilingi milioni 115,000,000 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa majosho matano katika kata za Kingale Mitaa ya Msui na Tampori, Serya Mtaa wa Chandimo, Suruke Mtaa wa Tungufu na Kondoa Mjini Mtaa wa Tumbelo chang’ombe. Hivyo basi, ninamshauri Mheshimiwa Mbunge kuwasiliana na kujadiliana na Mkurugenzi wa Halmashauri ili kama kuna haja ya mabadiliko ya maeneo ya ujenzi wa majosho yaweze kufanywa kulingana na vipaumbele vya wananchi na Halmashauri. Ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza: -

Je, kuna maamuzi mengine baada ya Kamati ya Mawaziri nane kurudisha kwa wananchi wa Itigi shamba la Kampuni ya Tanganyika Packers?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, shamba la iliyokuwa Kampuni ya Tanganyika Packers ni kituo cha kupumzishia mifugo kinachojulikana kwa jina la Kitaraka Holding Ground. Shamba hili linamilikiwa na Serikali tangu tarehe 1 Mei, 1955 na linatambulika kwa Na. 35 na Hati ya Kumiliki Ardhi Na. 15467 inayotaja ukubwa wa shamba kuwa ni ekari 45,000 (hekta 18,218.623) kwa ajili ya malisho na kutunzia mifugo (cattle holding ground).

Mheshimiwa Spika, Kamati ya Mawaziri nane wa kisekta ya kutatua migogoro ya matumizi ya ardhi katika vijiji 975 haijarudisha kwa wananchi wa Itigi shamba la iliyokuwa Kampuni ya Tanganyika Packers. Serikali imeelekeza ifanyike tathmini ya kina ya shamba la Kitaraka ili kubaini hali halisi kwa sasa kwa ajili ya kuwezesha Serikali kufanya uamuzi wa kumaliza mgogoro uliopo.
MHE. NDAISABA G. RUHORO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa soko la mnada wa ng’ombe wa Murusagamba?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, Mbunge wa Jimbo la Ngara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa miundombinu ya mnada wa mpakani wa Murusagamba umekamilika na ulihusisha ujenzi wa uzio, mazizi na ukarabati wa ofisi. Baada ya ujenzi kukamilika Wizara inaandaa utaratibu wa kuanza kuhamasisha wafanyabiashara na wafugaji kuanza kutumia mnada huo ili kufanikisha mauzo ya mifugo nje ya nchi na kuongeza maduhuli kwa Serikali Kuu na Halmashauri.
MHE. NG’WASI D. KAMANI aliuliza:-

Je, nini mkakati wa kuongeza nguvu kwenye uvuvi ili vijana wa Mkoa wa Mwanza na Kanda ya Ziwa wanufaike na Ziwa Victoria?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ng’wasi Damas Kamani, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuwawezesha wavuvi boti za kisasa kwa mkopo usio na riba kupitia Benki ya Kilimo Tanzania (TADB). Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na TADB inakamilisha taratibu za kutoa maboti 158 kwa mkopo kwa Vyama vya Ushirika 45, Vikundi vya Wavuvi 71 na watu binafsi 43 ambao wengi wao ni vijana. Aidha, katika Ukanda wa Ziwa Victoria, jumla ya Vyama vya Ushirika 20 kwa maana ya Mkoa wa Mwanza 14, Vikundi 17 kwa maana ya Mkoa wa Mwanza 10, na watu binafsi 17 kwa Mwanza wanne, wanatarajiwa kunufaika na mkopo wa maboti hayo.

Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali imetenga fedha kwa ajili ya miradi ya ufugaji samaki kwenye vizimba katika Ziwa Victoria kwa kuwawezesha vijana kupata pembejeo za ufugaji samaki kwa mikopo isiyo na riba. Aidha, jumla ya wanufaika 3,154 ambao wengi wao ni vijana wameainishwa kunufaika na mkopo huo ikijumuisha vikundi 67, kwa maana ya Mwanza 42, vyama vya ushirika 24, Mwanza 14; kampuni 10, kwa Mkoa wa Mwanza vitano; na watu binafsi 32, kwa Mkoa wa Mwanza 16 kutoka ukanda wa Ziwa Victoria.
MHE. PRISCUS J. TARIMO aliuliza:-

Je, Mwaka 2021 – Januari, 2022 Sekta ya Mifugo imeuza nyama nje ya nchi kwa asilimia ngapi na upi mkakati wa kuimarisha Sekta hii?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, jumla ya tani 10,415 za nyama zimeuzwa nje ya nchi zenye thamani ya dola za Kimarekani 42,500,994.90 ikilinganishwa na tani 1,774.29 za nyama zenye thamani ya dola za Kimarekani 4,290,000 zilizouzwa katika mwaka wa fedha 2020/2021. Ongezeko hili ni sawa na asilimia 492.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na mikakati mbalimbali ya kuimarisha tasnia ya nyama ikiwemo; kuvutia uwekezaji katika ujenzi wa machinjio za kisasa zinazokidhi viwango vya kimataifa ambapo hadi sasa, zipo machinjio sita tu zenye ithibati ya kuuza nyama nje ya nchi; kuimarisha mazingira ya ufanyaji biashara katika tasnia ya nyama kwa kupunguza tozo na kodi za usafirishaji wa nyama nje ya nchi; kuwajengea uwezo vijana waliohitimu vyuo vya mifugo kupitia vituo atamizi ili waweze kufuga kisasa na kuzalisha malighafi ya kutosha kwa ajili ya viwanda vya kuchakata nyama na kuboresha mbari za mifugo kupitia uhimilishaji, ugawaji wa madume bora na usambazaji wa mitamba ya ng’ombe wa nyama.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza: -

Je, lini soko la samaki Mbamba Bay litaanza kutumika?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Jimbo la Nyasa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa soko la samaki la Mbamba Bay unafanyika kwa awamu ambapo awamu ya kwanza ulianza mwezi Mei 2021 na kukamilka mwezi Machi, 2022. Katika awamu ya kwanza Serikali ilijenga jengo kuu ambalo lina vizimba au meza za kuuzia samaki. Kwa sasa, Serikali inaanza awamu ya pili ya ujenzi wa soko hilo ambao unahusisha ujenzi wa miundombinu ya maji safi, maji taka pamoja na choo. Aidha, zabuni ya ujenzi huo imeshatangazwa na kufunguliwa Tarehe 23 Mei, 2023. Kazi ya uchambuzi na tathmini ya nyaraka za zabuni inaendelea ili kumpata mzabuni wa kuanza kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali inatambua umuhimu wa soko hilo na litaanza kutumika tu mara tu baada ya ujenzi wa miundombinu hiyo kukamilika.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukarabati Shule za Msingi za zamani katika Wilaya za Ileje na Mbozi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Gerald Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule 2,147 shule za msingi kongwe nchini ambazo zilianzishwa kabla ya kupata Uhuru mwaka 1961. Hali ya miundombinu ya shule hizo ni mseto zikiwemo zenye hali nzuri na nyingine zenye miundombinu chakavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeanza kufanya tathmini ya hali ya miundombinu ya shule zote za msingi kupitia mradi wa BOOST ili kubaini mahitaji ya ujenzi wa miundombinu mipya ya shule na hali ya uchakavu wa miundombinu iliyopo. Tathmini hiyo imeanza mwezi Aprili, 2022 na itakamilika mwezi Julai, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo ya tathmini hiyo yatatumika kuandaa mpango wa uendelezaji na ukarabati wa miundomibinu ya Shule za Msingi kwa miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi mwaka 2025/2026.
MHE. ALLY J. MAKOA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara za mitaa ya Halmashauri ya Mji wa Kondoa kwa kiwango cha lami kupitia Miradi ya TACTIC?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Juma Makoa, Mbunge wa Jimbo la Kondoa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuendeleza Mpango wa Kuboresha Miundombinu ya Msingi katika Miji Nchini, Serikali kupitia Mradi wa Tanzania Cities Transforming Infrastructure and Competitiveness Project (TACTIC) utakaotekelezwa katika miji 45. Mradi huo utatekelezwa katika Halmashauri za Majiji, Manispaa na Miji kupitia mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia wenye jumla ya Dola za Kimarekani milioni 500, baada ya kukidhi vigezo vilivyowekwa na Benki ya Dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Mji wa Kondoa ni miongoni mwa miji 45 nchini ambayo imepewa kipaumbele cha kupata ufadhili wa Mradi wa Uboreshaji wa Miundombinu katika Miji. Aidha, Halmashauri hii ipo kwenye kundi la tatu lenye jumla ya miji 18 ambayo inatarajiwa kuanza kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa miradi iliyopendekezwa na Halmashauri husika katika mwaka wa fedha 2022/2023.
MHE. ASIA A. HALAMGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha kwa ajili ya kumalizia Miradi ya Afya iliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asia Abdukarimu Halamga, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Manyara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua mchango wa wananchi katika ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya kote nchini. Aidha, Serikali imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati nchi nzima katika kila jimbo. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali ilitenga fedha Shilingi bilioni 27.75 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati 555 ambapo jumla ya Shilingi bilioni 26.95 zilitolewa na Serikali kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2021/2022, jumla ya shilingi bilioni 38.2, zimetengwa kwa ajili ya kukamilisha maboma ya zahanati 763 yaliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi ambapo maboma 564 yanakamilishwa kwa fedha ya ruzuku ya Serikali na maboma 199 kwa fedha za halmashauri mapato ya ndani, ambapo jumla ya fedha shilingi bilioni 30.98 zimekwishatolewa mpaka sasa, ikijumuisha shilingi bilioni 26.92 ruzuku ya Serikali na shilingi Bilioni 4.06 mapato ya ndani ya halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga shilingi bilioni 15 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati 300.
MHE. SYLVESTRY F. KOKA aliuliza:-

Je, ni lini Mji wa Kibaha utakuwa Manispaa ambao kwa sasa ni Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sylvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri huanzishwa au kupandishwa hadhi kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa Sura ya 287 na 288 pamoja na Mwongozo wa Uanzishwaji wa Maeneo ya Utawala wa mwaka 2014 ambao umeainisha vigezo na taratibu zinazopaswa kufuatwa ili kuanzisha au kupandisha hadhi Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, ni kweli mapendekezo ya kupandisha hadhi Halmashauri ya Mji Kibaha kuwa Manispaa yaliwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Mapendekezo hayo yalifanyiwa uhakiki na timu ya wataalam kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI mwaka 2016 kati ya vigezo 20 Halmashauri ya Mji wa Kibaha ilikuwa imekidhi vigezo 15 sawa na asilimia 75 tu.

Mheshimiwa Spika, vigezo ambavyo havikuwa vimefikiwa na Mji wa Kibaha ni pamoja na idadi ya watu, idadi ya kata na mitaa, kutokuwa na mpango kabambe wa uendelezaji mji, kutofikia asilimia zinazohitajika za wakazi waliokuwa wameunganishwa na huduma ya maji. Hivyo, Halmashauri hii haikuweza kupandishwa hadhi kwa kuwa ililazimu kukidhi vigezo vyote kwa pamaoja kwa mujibu wa Mwongozo wa Kuanzisha Maeneo ya Utawala wa mwaka 2014 ili kupandishwa hadhi ya kuwa Halmashauri ya Manispaa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo za Halmashauri ya Mji wa Kibaha, Serikali kwa sasa inakusudia kuimarisha maeneo yaliyopo ili yaweze kutoa huduma zilizokusudiwa ikiwa ni pamoja na miradi ya maendeleo. Hivyo, ninashauri Halmashauri ya Kibaha, kujikita katika kuboresha zaidi huduma za wananchi.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA aliuliza:-

Je, fedha za Mfuko wa Jimbo zinaweza kutumika kununulia samani za Ofisi ya Jimbo? Na kama jibu ni hapana, samani hizi zinapaswa kununuliwa na nani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela mbunge wa Jimbo wa Lulindi kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, mfuko wa kuchochea maendeleo ya Jimbo ulianzishwa kwa Sheria Na.16 ya mwaka 2009. Fedha za Mfuko wa Jimbo ni mahususi kwa ajili ya kutekeleza miradi ya kijamii iliyoanzishwa na wananchi wa Jimbo husika.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri zilielekezwa kuwapatia Wabunge Ofisi kwa ajili ya shughuli zao ikiwa ni pamoja na samani kulinganaa na uwezo wao wa ukusanyaji mapato yao ya ndani. Nachukua fursa hii kuwasihi Wakurugenzi wa Halmashauri kushirikiana na Wabunge katika kutekeleza majukumu yao.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza:-

Je, ni lini Mji wa Geita utakuwa Manispaa kwa kuwa taratibu zote zimekamilika na imefikia viwango vya kupewa hadhi ya Manispaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais – TAMISEMI ilipokea mapendekezo ya kupandisha hadhi Halmashauri ya Mji Geita kuwa Manispaa. Mapendekezo hayo yalifanyiwa uhakiki na timu ya Wataalam Kutoka OR-TAMISEMI, kati ya vigezo 21 Halmashauri ya Mji wa Geita ilikuwa imekidhi vigezo 18 sawa na asilimia 85. Vigezo ambavyo havikuwa vimefikiwa na Mji wa Geita ni pamoja na kutokuwa na Mpango Kabambe wa uendelezaji Mji, eneo lililopimwa lisipungue asilimia 75 ya eneo lote kutofikia asilimia 75 zinazohitajika za wakazi waliokuwa wameunganishwa na huduma ya maji. Hivyo, Halmashauri hii haikuweza kupandishwa hadhi kwa kuwa ililazimu kukidhi vigezo vyote kwa pamoja kwa mujibu wa mwongozo wa kuanzisha maeneo ya utawala wa mwaka 2014 ili kupandishwa hadhi ya kuwa Halmashauri ya Manispaa.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-

Je Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea zaidi posho Madiwani na kuwalipa mishahara Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kazi kubwa inayofanywa na Waheshimiwa Madiwani pamoja na Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji katika kusimamia utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia hilo, Serikali inatafuta vyanzo vipya vya fedha ili kuongeza posho za Madiwani. Pamoja na hilo, Halmashauri kwa kutumia mapato yake ya ndani zinawajibika kutenga sehemu ya mapato hayo kwa ajili kuwalipa posho Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafungua Zahanati iliyopo Kijiji cha Nyakashengi Kata ya Businde ili iweze kutoa huduma kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Jimbo la Kyerwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Zahanati iliyopo kwenye Kijiji cha Nyakashengi, Kata ya Businde tayari imeshasajiliwa kwa usajili Na. 120780-2 kutoka Wizara ya Afya na kuanza kutoa huduma tangu tarehe 15/04/2022. (Makofi)
MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza:-

Je, ni lini Daraja la Mto Nduruma litakalounganisha Kata za Mlangarini, Nduruma na Bwawani Wilayani Arumeru litajengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Seif Swai Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga Shilingi Milioni 70 kwa ajili ya ujenzi wa daraja la mawe katika Mto Nduruma ili kuunganisha Kata za Mlangarini, Nduruma na Bwawani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TARURA itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara hii ili kuboresha mawasiliano ya Kata za Mlangarini, Nduruma na Bwawani.
MHE. JACKSON G. KISWAGA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi Shule ya Sekondari Kalenga iliyopo Kata ya Ulanda kuwa ya kidato cha tano na sita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Jackson Gedion Kiswaga Mbunge wa Jimbo la Kalenga, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maelekezo ya Serikali ni kuwa na Shule ya Kidato cha Tano na Kidato cha Sita katika kila Tarafa zikiwemo Tarafa zilizoko katika Jimbo la Kalenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatafuta fedha katika mwaka 2022/2023 za ujenzi wa bweni la kulalia wanafunzi ili kukamilisha vigezo vya kupandishwa hadhi ya kuwa na Kidato cha Tano na Kidato cha Sita.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO K.n.y MHE. YAHYA A. MHATA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga Kituo cha Afya katika Kijiji cha Mikuwa Kata ya Mnanje Wilayani Nanyumbu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahya Ally Mhata, Mbunge wa Jimbo la Nanyumbu, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepeleka fedha Shilingi Milioni 250 kwenye Kata ya Mnanje kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya ambapo Kijiji cha Mikuwa ni miongoni mwa vijiji vilivyomo kwenye Kata hiyo. Majengo yanayojengwa kwenye Kituo hicho ni jengo la kuhudumia wagonjwa wa nje (OPD), Jengo la maabara na kichomea taka. Majengo hayo yapo katika hatua ya umaliziaji ukiacha kichomea taka ambacho ujenzi wake ndiyo umeanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais – TAMISEMI tayari imekwisha wasilisha maombi Wizara ya Fedha na Mipango ya Shilingi Milioni 250 kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa wodi ya wazazi, chumba cha upasuaji na jengo la kufulia.
MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:-

Je, ni nini mpango wa Serikali kufanya asilimia 50 ya wanafunzi wanaojiunga na Kidato cha Tano katika shule za Kata watoke ndani ya Halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya Mbunge wa Jimbo la Meatu, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali kuchanganya wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali ili kujenga Utaifa, kuchanganya wanafunzi kunasaidia msawazo wa nafasi zilizopo ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa wanafunzi wote waliofaulu wanapata nafasi ya kujiunga Kidato cha Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutumia wanafunzi asilimia 50 kujiunga na Shule za Sekondari kutasababisha baadhi yao kukosa nafasi kwa kuwa siyo kila mchepuo unapatikana kwenye shule zilizopo katika Halmashauri husika.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuunga mkono wananchi wa Jimbo la Manonga kwa kuwasaidia kujenga madarasa mawili katika kila shule?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Said Gulamali, Mbunge wa Jimbo la Manonga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua changamoto ya mahitaji ya vyumba vya madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mradi wa SEQUIP imepeleka shilingi milioni 470 kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Sekondari Seif Gulamali. Pia katika mwaka 2021 kupitia mradi wa Mpango wa Maendeleo ya Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 jimbo la manonga lilipokea jumla ya shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 92 kwa shule za sekondari na shilingi milioni 160 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba nane vya madarasa ya shule za msingi shikizi.

Katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi milioni 200 kwa ajili ya ukamilishaji wa vyumba 10 vya madarasa katika Halmashauri ya Wilaya Igaunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa kadri zitakapopatikana.
MHE. DOROTHY G. KILAVE K.n.y MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa kiasi cha fedha ilizoahidi kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Malula Kibaoni hadi Ngerenanyuki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini imetenga kiasi cha Shilingi Bilioni Moja kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Malula - King’ori – Leguluki - Ngarenanyuki yenye urefu wa kilomita 33.7 kwa kiwango cha changarawe. Ujenzi wa Barabara hiyo umefikia asilimia 70 ambapo kazi zilizotekelezwa hadi sasa ni uchongaji wa barabara kilomita 33.7, karavati 16 na uwekaji wa tabaka la changarawe kilomita Tisa umekamilika na ujenzi unaendelea. Ujenzi huu unatarajiwa kukamilika Tarehe 28 Juni, 2022.
MHE. BONIPHACE M. GETERE K.n.y. MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza michango kwa Wanafunzi wanaojiunga Kidato cha Kwanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Kembaki Michael, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Waraka wa Elimu Namba 5 wa mwaka 2015 iliamua kutoa Elimu Msingi kuanzia Elimu ya Awali hadi Kidato cha Nne bila malipo. Azma hii ya Serikali ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 ambayo ina lengo la kuhakikisha kwamba watoto wote wa Kitanzania wenye rika lengwa la Elimu Msingi wanapata elimu bila kikwazo chochote ikiwemo ada au michango.

Mheshimiwa Spika, michango inayoendelea shuleni kwa sasa ni michango ya lishe ambayo imepata kibali cha Mkuu wa Wilaya baada ya kuidhinishwa na Mkutano Mkuu wa Wazazi. Michango hii ni kwa wanafunzi wote wa Kidato cha Kwanza hadi Kidato cha Nne.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka Watumishi wa Kada ya Afya Wilayani Kalambo kwa kuzingatia upungufu uliopo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephat Sinkamba Kandege, Mbunge wa Jimbo la Kalambo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka huu wa fedha imepanga kuajiri watumishi wa kada ya afya 7,612 watakaopangiwa katika Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo.
MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza:

Je, ni lini Serikali itajenga Shule za Sekondari katika Kata za Sasu, Nhwande, Makingi na Kanonge katika Jimbo la Ulyankulu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rehema Juma Migila, Mbunge wa Jimbo la Ulyankulu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha wa 2021/2022, Serikali imetuma fedha katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya za sekondari 15 kupitia mradi wa EP4R shilingi bilioni 15.0 na shule 232 kupitia mradi wa SEQUIP shilingi bilioni 109.57 katika kata ambazo hazina shule na maeneo ambayo yana wanafunzi wengi ukilinganisha na miundombinu ya shule zilizopo.

Mheshimiwa Spika, kati ya fedha zilizotumwa Jimbo la Ulyankulu limepokea fedha shilingi milioni 470 kwa ajili ya ujenzi wa shule moja ya sekondari ya kata. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kata zote zinakuwa na Shule za Sekondari nchini zikiwemo Kata za Sasu, Nhwande, Makingi na Kanonge ambapo kupitia Mradi wa SEQUIP jumla ya shule za sekondari 1,000 zinatarajia kujengwa nchini ili kuwapunguzia umbali wa kutembea wanafunzi kufuata shule.
MHE. VENANT D. PROTAS aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga daraja katika Mto Loya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venant Daud Protas, Mbunge wa Igalula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TARURA katika bajeti ya mwaka wa fedha 2021/2022 imetenga shilingi milioni 318.90 kwa ajili ya usanifu wa daraja la Mto Loya ambapo tayari kazi ya usanifu ilianza tarehe 22 Desemba, 2021 na inategemea kukamilika tarehe 21 Juni, 2022 ambapo gharama halisi za ujenzi zitakuwa zimejulikana. Kazi hiyo ya usanifu inafanywa na Mhandisi Mshauri Advanced Engineering Solutions ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kujulikana kwa gharama za ujenzi huo ambao unalenga kujenga daraja kubwa na daraja la watembea kwa Miguu ikiwa ni pamoja na kujenga barabara approach road yenye urefu wa kilometa 13, Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa soko la kisasa la Kwa Sadala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Hai imeandaa andiko la mradi wa ujenzi wa soko la Kwa Sadala wenye thamani ya shilingi bilioni tisa. Andiko hilo limefanyiwa uchambuzi na Mkoa ambapo mapungufu yaliyojitokeza yamewasilishwa Halmashauri kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, pindi marekebisho hayo, yatakapokamilika na kukidhi vigezo Serikali itatafuta fedha kutoka vyanzo mbalimbali kwa ajili ya kutekeleza mradi huo.
MHE. REGINA N. QWARAY aliuliza:-

Je, Serikali haioni haja ya kuongeza kiwango cha mikopo ya vikundi vya watu watano inayotolewa na Halmashauri kutoka shilingi milioni moja hadi shilingi milioni tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Regina Ndege Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kanuni ya 9 ya Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo kwa Vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu ya mwaka 2019 imeelekeza kwamba fedha za mikopo zitakazotolewa zitatumika kwa miradi iliyoidhinishwa na Kamati ya Kudumu ya Fedha, Mipango na Uongozi kwa kuzingatia ushauri na mapendekezo ya Timu ya Menejimenti na Kamati ya Huduma za Mikopo. Hivyo, ni jukumu la kikundi husika kuomba mkopo kulingana na mahitaji ya mradi husika.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA K.n.y MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukabiliana na changamoto ya uhaba wa walimu, madarasa, samani na miundombinu mingine inayochagizwa na utekelezaji wa Sera ya Elimu bila Malipo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima, Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua kukabiliana na upungufu wa walimu katika shule za msingi na sekondari nchini kwa kuajiri walimu na kuwapanga katika maeneo yenye uhaba, kufanya msawazo wa walimu katika maeneo yasiyo na walimu wa kutosha

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika kukabiliana na changamoto ya miundombinu ya elimu inaendelea kujenga shule mpya, madarasa yenye samani ndani yake na kuboresha miundombinu chakavu kupitia bajeti ya Serikali na miradi ya kuboresha elimu kama vile BOOST, SEQUIP, EP4R na GPE LANES II.
MHE. DEUS C. SANGU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami inayounganisha Mji Mdogo wa Mtowisa na Sumbawanga Mjini kupitia Mlima Ng’ongo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Jimbo la Kwela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, awali barabara hii ilisanifiwa kujengwa kwa kiwango cha changarawe kabla ya ahadi ya Mheshimiwa Rais kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami ambapo katika bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi milioni 875 kwa ajili ya kujenga urefu wa kilometa 25 kwa kiwango cha changarawe.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA K.n.y. MHE. DKT. DAVID M. DAVID aliuliza:-

Je kwa nini Serikali haitengi fedha za TARURA kwa kuzingatia jiografia, ukubwa wa eneo na mazingira ya Wilaya au Jimbo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA ZA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Jimbo la Same Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, TARURA inaendelea na zoezi la uandaaji wa formula itakayotumika kwenye ugawaji wa rasilimali fedha zinazohitajika kwenye ujenzi na matengenezo na miundombinu ya barabara kulingana na mahitaji ya eneo husika. Formula itazingatia ukubwa wa mtandao wa barabara (road network), thamani ya miundombinu ya barabara iliyopo (asset value), hali ya barabara (road condition), wingi wa magari (traffic volume), idadi ya wakazi (population), mazingira (geographical terrain), kiwango cha mvua (annual rainfall) na kilimo (agriculture potential).
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Maafisa Masuuli na Wahasibu katika Halmashauri wanapata mafunzo juu ya uandaaji wa taarifa za fedha za mwisho za halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetoa mafunzo kwa jumla ya watumishi 210 juu ya uandaaji wa taarifa za fedha za mwaka unaoishia tarehe 30 Juni, 2022. Mafunzo hayo yametolewa kwa watumishi waliopo ngazi ya mikoa na halmashauri zote nchini.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha Mwongozo wa Uhasibu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wa mwaka 2020 (Local Authority Accounting Manual) na Waraka wa Ufungaji Hesabu kila mwaka. Maboresho hayo yanakusudia kuzikumbusha taasisi za umma juu ya mambo ya msingi ya kuzingatia na kuwaongoza Maafisa Masuuli na Wahasibu katika kutekeleza majukumu yao ikiwa ni pamoja na uandaaji wa hesabu za mwisho.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa fedha za ujenzi wa barabara ya kilometa tatu kwa kuanzia katika Halmashauri ya Geita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Musukuma Joseph Kasheku, Mbunge wa Jimbo la Geita, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha Lami nyepesi kilomita moja katika eneo la Nzera.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango uliopo ni kuendelea kuweka kwenye mipango na bajeti ya kila mwaka ili kuweza kukamilisha ujenzi wa kilometa tatu ifikapo mwaka 2025.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza kutenga fedha za dharura kwa ajili ya barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TARURA imekuwa ikitenga fedha za dharura sawa na asilimia tano ya bajeti ya fedha za Mfuko wa Barabara. Katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi bilioni 11.45 kwa ajili ya fedha za dharura za matengenezo ya barabara nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha ya dharura kwa ajili ya kufanya matengenezo na ujenzi wa miundombinu ya barabara kulingana na upatikanaji wa fedha. Lengo ni kuboresha mtandao wa barabara unaohudumiwa na TARURA.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA aliuliza: -

Je, ni lini mradi wa barabara wa kilometa 96 unaofadhiliwa na Benki ya Dunia utafika Mbogwe?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Henry Nicodemas Maganga, Mbunge wa Jimbo la Mbogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Tanzania, kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) na Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS), inatekeleza Mradi wa Maendeleo ya Barabara kwa Ushirikishaji Jamii na Ufunguaji Fursa za Kijamii na Kiuchumi Vijijini (Roads to Inclusion and Socioeconomic Opportunities - RISE). Mradi huu utagharimu kiasi cha dola za Marekani milioni 350, ambapo, kiasi cha milioni 300 ni mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia na milioni 50 ni mchango wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe ni miongoni mwa Halmashauri zitakazonufaika na Mradi wa RISE ambapo jumla ya kilometa 96 zinaratajiwa kujengwa. Kwa sasa TARURA ipo kwenye hatua ya manunuzi ya Mtaalamu Mshauri wa kufanya usanifu wa kina (detailed engineering design) wa barabara zilizopendekezwa. Ujenzi unatarajiwa kuanza ndani ya mwaka wa fedha 2022/2023 baada ya usanifu kukamilika, ahsante.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuunga mkono wananchi wa Jimbo la Manonga kwa kuwasaidia kujenga madarasa mawili katika kila shule?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Said Gulamali, Mbunge wa Jimbo la Manonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua changamoto ya mahitaji ya vyumba vya madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mradi wa SEQUIP imepeleka shilingi milioni 470 kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Sekondari Seif Gulamali. Pia katika mwaka 2021 kupitia mradi wa Mpango wa Maendeleo ya Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 jimbo la manonga lilipokea jumla ya shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 92 kwa shule za sekondari na shilingi milioni 160 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba nane vya madarasa ya shule za msingi shikizi.

Katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi milioni 200 kwa ajili ya ukamilishaji wa vyumba 10 vya madarasa katika Halmashauri ya Wilaya Igaunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa kadri zitakapopatikana.
MHE. DANIEL T. AWACK aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya ujenzi wa barabara za ndani za kilometa 10 katika Mji wa Karatu kwa kiwango cha lami iliyotolewa na Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. John Pombe Magufuli?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Tlemai Awack, Mbunge wa Jimbo Karatu, kama ifuatvyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 barabara NBC - Kudu yenye urefu wa kilometa 0.6 ilijengwa kwa gharama ya shilingi milioni 350. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, ujenzi wa barabara za Tarafa - Ari Mpya, TRA - Mahakamani na NBC - Kudu zenye urefu wa kilometa 0.9 kwa gharama ya shilingi milioni 499.99 ambapo hadi sasa utekelezaji wake umefikia asilimia 78 na zinatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2022.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa barabara za Canivo - Buchani kilometa 0.53; Posta - Maliasili kilometa 0.10 na Bambras - Continental kilometa 0.100 zenye jumla ya urefu wa kilometa 0.73 zinaendelea kutekelezwa ambapo hadi sasa utekelezaji wake umefikia asilimia 70. Kwa upande wa mwaka wa fedha 2022/2023 jumla ya shilingi milioni 500 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara kilometa 0.62 kwa kiwango cha lami kwa barabara za Gorwa, Posta – Mailimbili, Bampras Continental na Rhotia Pharmacy. Serikali itaendelea kutekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa barabara za Mji wa Karatu kwa kiwango cha lami kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. DOROTHY G. KILAVE aliuliza: -

Je, Serikali ina mikakati gani ya kupanua wigo wa miradi ya kuboresha barabara za mitaa ya Manispaa ya Temeke hasa Jimbo la Temeke kupitia DMDP?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy George Kilave, Mbunge wa Jimbo la Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mradi wa DMDP Awamu ya Kwanza inajenga mtandao wa barabara wenye jumla ya kilometa 48.243 kwa gharama ya shilingi billion 60.9 katika Jimbo la Temeke kwa Kata za Mtoni kilometa 9.623; Makangarawe kilometa 10.402; Yombo vituka kilometa 7.710; Kilakala kilometa 10.53; Keko kilometa 0.462; Buza kilometa 1.7; na Kata za Changombe, Sandali, Temeke na Azimio zimejengwa kilometa 7.8. Kwa sasa kilometa 46.543 zimekamilika na zinatumika na kilometa 1.7 za Buza zilizosalia zinatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Septemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, kupitia Mradi wa DMDP Awamu ya Pili katika Jimbo la Temeke imependekezwa kujengwa mtandao wa barabara wa jumla ya kilometa 53.10 kwa kiwango cha lami zinazokadiriwa kugharimu shilingi billioni 69.5. Ofisi ya Rais – TAMISEMI imewasilisha mapendekezo hayo Wizara ya Fedha na Mipango ili iwe sehemu ya mzunguko wa 20 wa mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia katika Mkoa wa Dar es Salaam unaotarajia kuanza mwezi Julai, 2022.
MHE. DOROTHY G. KILAVE K.n.y MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa kiasi cha fedha ilizoahidi kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Malula Kibaoni hadi Ngerenanyuki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini imetenga kiasi cha Shilingi Bilioni Moja kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Malula - King’ori – Leguluki - Ngarenanyuki yenye urefu wa kilomita 33.7 kwa kiwango cha changarawe. Ujenzi wa Barabara hiyo umefikia asilimia 70 ambapo kazi zilizotekelezwa hadi sasa ni uchongaji wa barabara kilomita 33.7, karavati 16 na uwekaji wa tabaka la changarawe kilomita Tisa umekamilika na ujenzi unaendelea. Ujenzi huu unatarajiwa kukamilika Tarehe 28 Juni, 2022.
MHE. BONIPHACE M. GETERE K.n.y. MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza michango kwa Wanafunzi wanaojiunga Kidato cha Kwanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Kembaki Michael, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Waraka wa Elimu Namba 5 wa mwaka 2015 iliamua kutoa Elimu Msingi kuanzia Elimu ya Awali hadi Kidato cha Nne bila malipo. Azma hii ya Serikali ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 ambayo ina lengo la kuhakikisha kwamba watoto wote wa Kitanzania wenye rika lengwa la Elimu Msingi wanapata elimu bila kikwazo chochote ikiwemo ada au michango.

Mheshimiwa Spika, michango inayoendelea shuleni kwa sasa ni michango ya lishe ambayo imepata kibali cha Mkuu wa Wilaya baada ya kuidhinishwa na Mkutano Mkuu wa Wazazi. Michango hii ni kwa wanafunzi wote wa Kidato cha Kwanza hadi Kidato cha Nne.
MHE. BONIPHACE M. GETERE K.n.y. MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza michango kwa Wanafunzi wanaojiunga Kidato cha Kwanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Kembaki Michael, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Waraka wa Elimu Namba 5 wa mwaka 2015 iliamua kutoa Elimu Msingi kuanzia Elimu ya Awali hadi Kidato cha Nne bila malipo. Azma hii ya Serikali ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 ambayo ina lengo la kuhakikisha kwamba watoto wote wa Kitanzania wenye rika lengwa la Elimu Msingi wanapata elimu bila kikwazo chochote ikiwemo ada au michango.

Mheshimiwa Spika, michango inayoendelea shuleni kwa sasa ni michango ya lishe ambayo imepata kibali cha Mkuu wa Wilaya baada ya kuidhinishwa na Mkutano Mkuu wa Wazazi. Michango hii ni kwa wanafunzi wote wa Kidato cha Kwanza hadi Kidato cha Nne.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA aliuliza:-

Je, lini Serikali itajenga miundombinu ya umwagiliaji katika mabonde ya mpunga ya Kwamgumi na Kwamsisi - Korogwe?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa Niaba ya Waziri wa Kilimo, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alfred James Kimea, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Korogwe ina zaidi ya skimu 64 zilizoendelezwa na ambazo hazijaendelezwa ikiwemo Skimu ya Kwamgumi inayokadiriwa kuwa na ukubwa wa hekta 210 na Kwamsisi yenye ukubwa unaokadiriwa kufika hekta 1,500.

Mheshimiwa Spika, katika skimu ya Kwamgumi Serikali imefanya uwekezaji wa awali kwa kufanya ujenzi wa mfereji mkuu wenye urefu wa kilomita tatu. Aidha, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imefanya ukaguzi na tathmini ya awali kwa ajili ya kufanya ukarabati na uendelezaji wa miundombinu ya umwagiliaji katika skimu hii, ikiwemo usakafiaji wa mifereji ya kupitisha maji kwa ajili ya umwagiliaji. Hivyo basi, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa Skimu ya Kwamgumi utaingizwa katika mpango na bajeti ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika mwaka wa fedha 2024/2025.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ina mpango wa kujenga miundombinu katika Skimu ya Kwamsisi. Aidha, mchakato wa manunuzi kwa ajili ya kumpata Mkandarasi wa kufanya ujenzi katika skimu hii umeanza.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, kuna mpango gani wa kuongeza mnyororo wa thamani wa zao la Kahawa ikiwa ni miongoni mwa mikakati ya kukuza soko la Kahawa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Tasnia ya Kahawa inatekeleza mkakati wa miaka mitano wa Maendeleo ya Tasnia ya Kahawa (2021 - 2025). Moja ya malengo ya mkakati huo ni kuongeza thamani ya kahawa kutoka 7% za sasa mpaka 15% ya kahawa yote inayozalishwa nchini.

Mheshimiwa Spika, katika kupunguza utegemezi wa soko la nje, Serikali imeweka mazingira mazuri ya kuvutia uwekezaji kwenye viwanda vya kuongeza thamani ya kahawa kwa ngazi ya tatu na ngazi ya nne (tertiary processing).

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Bodi ya Kahawa kwa kushirikiana na Sekta Binafsi iliweka lengo la kuzalisha miche bora ya kahawa milioni 20. Hadi kufikia Juni, 2023 miche 17,866,980 ya kahawa sawa na 89% ya lengo ilizalishwa. Miche hiyo imeanza kusambazwa kwa ajili ya wakulima katika maeneo yanayopata mvua za vuli.