Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Joseph Osmund Mbilinyi (23 total)

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika jibu lake la msingi Mheshimiwa Waziri amesema kwamba amewashauri walionunua viwanda ambao wameshindwa kuviendeleza chini ya sera ya ubinafsishaji watafute wabia, lakini wote tunakumbuka Serikali hii wakati wa kampeni na hata baada ya kampeni mara kadhaa imetoa matamko kwamba itawapa muda wawekezaji walioshindwa kuviendeleza viwanda wavirudishe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijue Kiwanda cha ZZK Mbeya, Kiwanda cha Chai Katumba na Mbeya Textile, ni lini vitarudishwa kama ambavyo mliahidi kwenye kampeni na baada ya uchaguzi au hizi ndiyo siasa za flip flap?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbilinyi, Chief Lumanyika kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hotuba yangu haya maneno mengine mimi siyo mtu wa rahisi rahisi siwezi kuteka mtu nyara. Kuna mambo mawili, kiwanda ulichopewa natumia lugha viwanda vilivyobinafsishwa havikuuzwa, walipewa. Kwa sababu ile pesa waliolipa ilikuwa na masharti kwamba ukiendeleze kizae bidhaa, uzalishe bidhaa, utoe ajira na ulipe kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la Mheshimiwa Mwijage nimezungumza lazima mtu alipe kodi, sasa habari yenyewe ndiyo hii, tamko la Serikali ni hili. Aliyepewa kiwanda kwa utaratibu huo, ama kiendeshwe ama atapewa mtu mwingine akiendeleze, mambo ya kujadiliana hayo hayapo, na imeandikwa kwenye hotuba yangu. Nimekuwa nikilisema nimeliandika kwenye hotuba yangu nitakuwa kwenye position ya kuwaeleza kabla ya nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha unaoanza kwamba hizi ni mbivu, hizi ni mbichi, lakini lakini viwanda vyote viwe vinafanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaeleze tu kwamba wote waliochukua viwanda wanakuja kwa Msajili wa Hazina na wametoa programu namna ya kutengeneza, programu siyo moja. Hili suala ni la kimakataba, wanamikataba tunahakikisha kwamba tunakwenda kwa mikataba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna viwanda vingine vilishindwa kufanyakazi kwa sababu ya ushindani usio sawa, ndiyo maana tunaweka mazingira wezeshi kwa kuzuia watu waliokuwa wana-dump bidhaa hapa. Ni kama maswali mnayolalamikia kwamba kuna uplifting, uplifting zitaendela ili kuwazuia watu wanao-dump vitu hapa kusudi viwanda vyangu vifanye kazi.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumzia sana kuhusu kuwawezesha wakulima ili waweze kujenga viwanda, lakini pia amekiri kwamba pembejeo ni bei ghali sana kwa wakulima wetu. Sasa nikijaribu kuangalia bajeti iliyopita juzi tu kwa Wizara hii, bajeti ya mbolea imeshuka shilingi bilioni plus, imekwenda mpaka around shilingi bilioni 20.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa gap hiyo ya kushuka kwa bajeti ya mbolea kutaenda kuondoa ukali wa bei kwenye mbolea na kutawasaidia vipi wakulima kuondokana na kuzalisha katika hali ngumu sana na kuendelea kuwa maskini? Vinginevyo tutakuwa tunaendelea kupiga porojo tu hapa.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Pamoja na ukweli kwamba katika bajeti kulikuwa na changamoto kuhusiana na fedha za pembejeo, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara kwa sasa inaandaa utaratibu mpya wa kutoa ruzuku katika pembejeo ambao utaruhusu wakulima wengi zaidi kuliko ilivyo sasa kuweza kunufaika na ruzuku na kwa bei nafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utaratibu wa sasa, wote mmesikia malalamiko kwamba pamoja na kwamba Serikali ilitoa fedha nyingi, kwa mfano, katika mwaka wa fedha unaokwisha Serikali ilitoa shilingi bilioni 78 kwa ajili ya ruzuku, lakini mnafahamu utaratibu unaotumika sasa unaowafanya wachache wanufaike na mara nyingi ruzuku ile haiendi kwa wananchi. Sasa Serikali inakuja na utaratibu ambao inawezekana kwamba mbolea zote zikawa na ruzuku na zikapatikana nchini kama tunavyosema, kama bidhaa nyingine na siyo kwa wakulima mmoja mmoja.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, pamoja na changamoto iliyopo, haitaathiri nia ya Serikali na uwezo wa Serikali kuweza kuwapatia wananchi pembejeo kwa bei nafuu.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: nakushukuru sana dada yangu Mheshimiwa Naibu Spika na Mbunge wa Viti Maalum Kinondoni. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Wamachinga siyo eneo, ni mazingira ya biashara. Nimekuwa nalisema hili mara zote. Ndiyo maana tulikuwa wakati ule tukisafiri kwenda China, Beijing, mimi kazi ya kwanza naangalia mazingira ya Wamachinga, wapo hawapo? Unakuta wapo. Ukienda New York unaangalia Wamachinga; wapo? Unakuta wapo. Kinachotakiwa ni mazingira ya kibiashara.
Mheshimiwa Waziri, naomba ukae kidogo. Kwa ajili ya kuweka kumbukumbu sawasawa, mimi ni Mbunge wa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais, sio Mbunge wa Viti Maalum. Kwa hiyo, lazima kumbukumbu zikae sawasawa.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mbilinyi, kwamba tatizo la wafanyabiashara wadogo wadogo wanaojulikana…(Kelele)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimemwelewa Mheshimiwa Mbilinyi kwamba Wamachinga tatizo lao siyo kuwajengea, ila tatizo lao ni mazingira yanayofaa kwa biashara zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nami nataka nikubaliane naye kabisa kwa sababu Wamachinga hata ukiwajengea sehemu nzuri namna gani, kwa sababu wateja wa Wamachinga wanajulikana. Kama wateja wale hawafiki, ni kazi bure. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niziombe Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini, Mheshimiwa Rais amesema wasibugudhiwe hawa; maana yake nini? Watafutiwe maeneo yanayofaa kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge; yanayofaa kwa shughuli zao. Kwa hiyo, naweza kusema nimeelewa swali la Mheshimiwa Mbunge na kwamba Mamlaka za Serikali za Mitaa zinafahamu wajibu wao na zilikwishaelekezwa na Mheshimiwa Rais alikwishasema kwamba watengewe maeneo yanayofaa kwa shughuli zao.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema mnyonge mnyongeni haki yake mpeni, napenda niipongeze Serikali kwa kukubali kwamba kuna tatizo la utesaji na torture kwa sababu siku hizi kumekuwa na utaratibu na utamaduni wa kukataa na kukanusha kila kitu. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kukubali kwamba kuna tatizo la utesaji na torture. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali langu limejibiwa kwa wepesi na ujumla sana. Kwenye swali langu la msingi nili-cite kwa mfano, kinachoendelea kuhusu Mwalimu Msigwa na wenzake ambao walimfanyia torture au shambulio la kudhuru mwanafunzi wa Mbeya Sekondari ambapo mpaka leo hii wazazi wana hofu na watoto wao katika shule ile kiasi kwamba wanamsukuma Mbunge kutaka kujua ni nini hatma ya wale walimu kwa sababu maneno yamekuwa mengi. Mara wanasema amri kutoka juu imesema kwamba waachiwe na kadhalika...
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejiuliza sana na juzi nimeuliza kwenye Kamati lakini Waziri wa Elimu anasema hana habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimeuliza kwenye Kamati wanasema chuo kimeunda tume, chuo kinafanya uchunguzi wa jinai toka lini wakati suala hili liko wazi kwenye video ilienda viral wale walimu walitesa watoto tunawatetea walimu lakini wanapovunja sheria ni lazima hatua zichukuliwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka kujua ni nani aliyetoa amri kwamba wale walimu waachiwe wasichukuliwe hatua za kisheria kwa kosa la jinai walilofanya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Watanzania wanaowatesa wenzao ni pamoja na Polisi. Watanzania hawa Polisi, kwa mfano wakati wa Operesheni UKUTA ambayo tuliisitisha kwa maslahi ya Taifa, walikamata watu, waka-torture mfano Mtanzania Nyagali maarufu kama Mdude wa Mbozi ambaye mpaka leo hii amevunjwa miguu na hayuko sawasawa. Sasa Taifa hili limekuwa Taifa la disappearance watu wanapotea...
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijue kwa nini isiundwe Tume ya Kimahakama kama ile aliyounda Mheshimiwa Kikwete ya kuchunguza Operesheni TOKOMEZA ili kuchunguza maovu haya yanayofanywa na Watanzania ambao wana uniform za kipolisi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la walimu ambao wamewanyanyasa wanafunzi kwenye shule ya Mbeya Day niseme ni mtambuka kwa hiyo hatua mbalimbali zinachukuliwa na mamlaka husika. Kwa upande wa Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Mashtaka DPP kuna hatua ambazo zinaendelea kuchukuliwa na pale ambapo ushahidi na uchunguzi utakapokamilika watafikishwa katika vyombo vya sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni kuhusu kuundwa Tume ya UKUTA, kwanza tulishazungumza mapema kwamba mkusanyiko wowote ambao si halali hautaruhusiwa na hivyo Jeshi la Polisi litasimamia kuhakikisha kwamba linalinda usalama wa nchi hii kwa kuzuia mikusanyiko yoyote ambayo siyo halali. Kwa hiyo, kama ikiwa Jeshi la Polisi limetekeleza majukumu yake kuzuia mkusanyiko ambao si halali limefanya hivyo katika kutekeleza majukumu ya kawaida na tunawasihi wananchi pale wanapoelekezwa kutii sheria za nchi, basi watii sheria za nchi.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa wokovu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wakati maeneo mengi tatizo ni miundombinu na vyanzo vya maji, Mbeya hatuna tatizo la kati ya hayo kwa maana ya vyanzo vya maji, hatuna au hatutakiwi kuwa na tatizo la vyanzo vya maji; lakini pia miundombinu Mbeya ilishakamilika mwaka 2013 ikazinduliwa na Rais Mstaafu, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete mradi ambao ulifadhiliwa kwa mabilioni na EU. Leo hii pamoja na yote hayo, tuna wiki ya nne, takriban mwezi mzima Mbeya maji hayatoki kuanzia Uyole kwenda Mwakibete, Mama John na Sai, maji hayatoki kote.
Mheshimiwa Spika, naomba Waziri wa Maji asimame hapa awaambie wana Mbeya anatusaidiaje kutuokoa kwa sababu tupo kwenye hatari ya kukutana hata na magonjwa ya milipuko ukizingatia hiki ni kifuku, mvua zinanyesha, halafu maji ya kufanya usafi hamna. Kwa kweli Mbeya ni disaster na inahitaji neno la haraka sana kutoka kwa Waziri Mheshimiwa Engineer Lwenge.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, swali la Mheshimiwa Sugu kuhusiana na matatizo ya maji katika Mji wa Mbeya; wiki iliyopita ilinyesha mvua kubwa sana Mbeya ya muda mfupi lakini ilikuwa mvua kubwa. Maji yalitiririka yakaenda mpaka kwenye chanzo cha Nzogwe sehemu ambayo ina pampu zinazosukuma maji katika Mji wa Mbeya.
Mheshimiwa Spika, kutokana na hilo, kwa sababu zile pampu zinatumia umeme na kwa teknolojia, kukiwa na maji huwezi kuwasha umeme, kwa hiyo Mji wa Mbeya umekosa maji kwa muda wa siku nne. Taarifa hii kabla Mheshimiwa Sugu hajasema, nilikuwa nimetaarifiwa tayari na Mheshimiwa Mwanjelwa kwamba Mji wa Mbeya una matatizo.
Mheshimiwa Spika, jana tatizo hilo lilikamilika, baadhi ya mashine zikawashwa; na leo asubuhi mashine zilizobaki tayari zimeshawashwa. Kwa hiyo, nakuomba tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tukitoka Bungeni saa 7.00 naomba upige simu tena utakuta hali ya maji tayari imeshakaa vizuri.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili limerudi mara ya pili, lililetwa mwaka 2016 na majibu yalikuwa tofauti. Mwaka 2016 waliniambia fedha ziko tayari kwa ajili ya upanuzi wa barabara ya Uyole ya TANZAM, lakini leo wananiambia upanuzi utaanza pale upembuzi yakinifu na usanifu utakapopatikana na kuonesha viwango vya upanuzi vinavyohitajika na Serikali itakapopata fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 waliniambia fedha tayari ipo. Sasa hili ni tatizo, mara wanahama kutoka
project hii ambayo tulikuwa tumeshaizungumzia, wanarukia project nyingine wakati wameshasema fedha hakuna. Kwa nini upembuzi unafanywa na TAMISEMI badala ya TANROADS?
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwape ushauri kwamba efforts ziwekwe kwenye kupanua barabara kuu inayopita
Mwanjelwa ya TANZAM iwe ya four lanes kwa sababu mchakato wake umeshaanza, nyumba za wananchi zimeshavunjwa, wengine wamevunja kwa hiyari na wengine wanasubiri fidia huu ukiwa mwaka wa pili sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, mtachukua ushauri wangu kurudisha efforts kwenye barabara kuu ya
TANZAM kwa sababu tayari mchakato wake ni kama umeshaanza na ule mchakato mwingine ni kama kuanza
upya?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Mheshimiwa Naibu Waziri kila anapokuja kujibu swali lililoulizwa na Mbunge wa
Upinzani hasa CHADEMA huwa anapenda kusema hata Mbunge fulani wa Viti Maalum wa CCM aliuliza hilo swali?
Mfano, akiuliza Msigwa utamtaja Mheshimiwa Ritta Kabati, nikiuliza mimi utamtaja Mheshimiwa Mary Mwanjelwa? Kwa nini unapenda ku-undermine shughuli za Wabunge wa Upinzani ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri
wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ambaye yupo katika sherehe ya uzinduzi wa ujenzi wa reli ya standard gauge,
naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph Mbilinyi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie kwamba Wizara hii inachapa kazi na Serikali hii kila inachoamua kutekeleza na inachokisema inamaanisha hicho. Naomba nirudie kwenye jibu langu la msingi kwamba
kazi ya usanifu pamoja na upembuzi itakapokamilika, suala la fedha litashughulikiwa na kazi hiyo itaanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba nimhakikishie kwamba ushauri wake umefika, tutawasilisha kwa wataalam
wakaufanyie kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nyongeza tu, mimi bahati mbaya huwa nasema ukweli. Sasa kama Mbunge wa
Viti Maalum amelishughulikia hilo hilo, nadhani ni sahihi naye kusema kwa sababu ninachokisema ni ukweli.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naibu Waziri ametaja miradi mingi veryambitious lakini ukweli ni kwamba kwenye Balozi zetu kuna ukata sana kiasi kwamba kuna Balozi zinawakilisha nchi kadhaa, mfano Balozi wa Malaysia anawakilisha mpaka Singapore na Brunei, wa Msumbiji nadhani mpaka Swaziland lakini wanashindwa kutembelea nchi wanazoziwakilisha kwa sababu ya ukata kiasi kwamba hata Ubalozi umekuwa sio deal tena.
Mheshimiwa Spika, Naibu Waziri amezungumzia tu infrastructure lakini hawajazungumzia hali za Mabalozi wenyewe na staff. Sasa Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba wanaboresha masuala ya kibajeti na kifedha kwenye Balozi zile ambazo zinawakilisha nchi kadhaa ili kutokuathiri mahusiano yetu ya kibalozi na zile nchi ambazo wanatakiwa hawa watu wakatuwakilishe?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme tu kwamba mtu anapoteuliwa kwenye utumishi wa umma sio deal ni wajibu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la pili kuhusu kusema kwamba tutakarabati sehemu mbalimbali na tumeweka miradi mingi lakini inaonekana baadhi ya Balozi zinasimamia nchi nyingi sana na kwamba kuna ukata. Sisi kama Serikali mipango yetu inatokana na ukusanyaji wa mapato ya kodi zilizoko ndani ya nchi husika. Kama Wizara, bajeti yetu inapangwa kutokana na ukomo wa bajeti tunaopewa.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi tutakuwa tunahakikisha kwamba pesa tunazopewa na hata tunavyozigawa, hatugawi kwa aina moja kwa maana ya hela zinazofanana, inategemea Balozi anasimamia nchi ngapi na gharama za uendeshaji wa maisha katika nchi husika yakoje. Ndiyo maana unakuta katika mwaka huu wa fedha tumeanzisha Balozi nyingine sita ili kuhakikisha kwamba tunapunguza mzigo wa usimamizi wa Balozi kwa nchi husika.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Hizi kilomita 10 Mheshimiwa Rais aliahidi maeneo mengi sana. Nashauri data zote za kilomita 10 ambazo Mheshimiwa Rais aliahidi ili wamkumbushe kwa sababu kwa Jiji langu la Mbeya aliahidi pia kilomita ikiwemo barabara ya Mapelele, Kata ya Ilemi lakini mpaka leo hatuoni mchakato wowote na hatujapata nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Rais kwa sababu hajawahi kuja Mbeya toka amechaguliwa zaidi anarudi tu Kanda ya Ziwa. Mara ya mwisho ilikuwa aje Mbeya juzi kwenye ALAT, lakini waka-cancel siku mbili kabla ya siku ya ALAT kufanyika…
Kwa hiyo, tunamwomba sana Mheshimiwa Rais aje Mbeya pia.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la rafiki yangu Mheshimiwa Sugu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunazo takwimu zote za nchi nzima za ahadi za Mheshimiwa Rais za ujenzi wa miundombinu ya lami lakini na maeneo mengine. Mheshimiwa Sugu anafahamu pale katika Jiji la Mbeya kupitia Ofisi yetu tumepata investment kubwa ya kujenga barabara za lami katika Jiji la Mbeya. Siyo barabara za lami peke yake tumefanya uboreshaji, zile barabara zote tunazifunga taa na kujenga damp za kisasa kupitia mradi wa Strategic City Project.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, jambo hili ni commitment ya Serikali na tumefanya vizuri Jiji la Mbeya, Tanga na Arusha na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba ahadi zote ambazo Mheshimiwa Rais alizizungumza katika Halmashauri mbalimbali tutazitekeleza kupitia miradi yetu na kuhakikisha kwamba ikifika 2020 viporo hivi tutakuwa tumevimaliza hakuna shida ya aina yoyote.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Bado niko kwenye aircraft, kwenye tiketi za ATCL kuna picha ya ndege aina ya Embraer ambayo inabeba abiria 105 ambayo kimsingi bado haipo nchini, lakini kwenye tiketi za ATCL wameweka picha ambayo inaonekana kama ndege ipo na ukinunua ile tiketi unaweza ukafikiri kwamba unaenda kupanda aircraft hiyo ya abiria 105 lakini ukienda kule unakuta na bombardier ya abiria 70.
Sasa kwa nini Serikali inafanya udanganyifu? Haihofii kwamba iko siku atatoka mtu mwenye upeo wake akaenda pale akakuta anapandishwa ndege ambayo haipo picha kwenye tiketi alafu aka-sue ndege ikakamatwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE):
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kwenye tiketi alizozizungumza hiyo picha bado ipo, lakini yale ni matoleo ya tu ya kawaida ambayo kikawaida kibiashara hayawezi kuathiri kabisa shughuli za utaratibu wa biashara ya usafishaji wa abiria kwa njia ya ndege. Hata hivyo, tutaliangalia na kuangalia namna ya kuweza kulirekebisha katika muda mfupi ujao. (Makofi)
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Suala la biashara ya vyuma chakavu inaonesha ni wazi kuna soko zuri la chuma nchini na nje ya nchi. Sasa kifupi tu, sijui mradi wa chuma Liganga na Mchuchuma umefikia wapi ili nchi ifaidike na soko hilo? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Mchuchuma na Liganga; katika mpango wa Serikali wa miaka mitano wa ujenzi wa uchumi wa viwanda, mchuma na Liganga ipo. Nilipofikia mimi; hili suala liko mezani kwangu. Nimepitia vivutio vyote vya mwekezaji alivyoweka, nimevikamilisha, vinakwenda kwenye mamlaka kusudi waweke sahihi, mwekezaji yuko tayari kuweka fidia na kuweza kuanza. Nikipata sahihi ya mamlaka tunaanza kazi.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na matatizo ya usikivu pia TBC kuna matatizo ya weledi kwa watangazaji. Mfano, kuna watangazaji wa TBC walitangaza uongo kwamba Donald Trump alimpongeza President Magufuli, upambe uliopitiliza mpaka tajiri anashtuka. Sasa wale watu walisimamishwa lakini hivi karibuni nimeanza kuwaona kwenye tv. Walipewa adhabu gani ili wasirudie tena upambe? (Kicheko)
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tulichukua hatua za kinidhamu kwa kosa ambalo ni la kiufundi tu ambalo mtu yeyote duniani hapa anaweza kulifanya. Yametokea matatizo kama hayo hayo Kenya yalifanyika na watangazaji wamerudi, tulichokifanya ni kuchukua tu hatua ya muda mfupi. Wazungu wanasema it’s a deterrent kwamba uwe muangalifu zaidi. Ni kitu kinafanyika kila siku. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii nikikuletea, tuchukulie tu mfano wa magazeti yote yanayochapishwa kila siku, ninakuhakikishia asilimia 60 utakuta kuna matatizo/makosa ndani, ni kitu cha ubinadamu. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na posho za ration allowance kuwa ndogo lakini pia inasemakana kuna mpango wa kuzifuta posho hizi ili askari wasipewe cash wawe wanakula ration makambini. Je, ni kweli?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, posho ya ration tutambue madhumuni yake kwanza, madhumuni ya posho ya ration ni kumlisha askari na maafisa ili waweze kutekeleza majukumu yao. Sasa wako wale ambao wako kwenye makambi, wako wale ambao wanalazimika kula ili waweze kutekeleza majukumu yao, hao kuna wazabuni katika Makambi yote wanaopewa fedha hizo ili waweze kuwalisha, lakini wale ambao majukumu yao hayapo katika Kambi wao wanapewa fedha zao taslimu ili waweze kutumia wanavyoamua wao wenyewe.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na matatizo ya usikivu pia TBC kuna matatizo ya weledi kwa watangazaji. Mfano, kuna watangazaji wa TBC walitangaza uongo kwamba Donald Trump alimpongeza President Magufuli, upambe uliopitiliza mpaka tajiri anashtuka. Sasa wale watu walisimamishwa lakini hivi karibuni nimeanza kuwaona kwenye tv. Walipewa adhabu gani ili wasirudie tena upambe? (Kicheko)
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tulichukua hatua za kinidhamu kwa kosa ambalo ni la kiufundi tu ambalo mtu yeyote duniani hapa anaweza kulifanya. Yametokea matatizo kama hayo hayo Kenya yalifanyika na watangazaji wamerudi, tulichokifanya ni kuchukua tu hatua ya muda mfupi. Wazungu wanasema it’s a deterrent kwamba uwe muangalifu zaidi. Ni kitu kinafanyika kila siku. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii nikikuletea, tuchukulie tu mfano wa magazeti yote yanayochapishwa kila siku, ninakuhakikishia asilimia 60 utakuta kuna matatizo/makosa ndani, ni kitu cha ubinadamu. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mheshimiwa Waziri amesisitiza mara kadhaa kwamba tuwe na desturi ya kupima, ni kitu kizuri kwa sababu UKIMWI bado upo na sometime unaona kama umezoeleka hivi. Ni kwa nini sasa vile vipimo (disposable) haviko kwenye maduka ya dawa ya kawaida ili hayo maelekezo ya Waziri anayoyasema kwamba tuwe na desturi ya kupima iwe rahisi? Kwa sababu yale mambo ya kusema kwamba mtu atazimia ni ya kizamani. Ni vizuri vipimo vya UKIMWI viwe available madukani kama ilivyo kwa vipimo vya sukari, pressure na kadhalika ambavyo viko available madukani. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni swali zuri na nieleze tu kwamba, katika hizi USD milioni 526 tulizopewa na Serikali ya Marekani kwenye mwaka huu wa fedha unaokuja, tumeweka mkakati wa kufanya majaribio ya self-test hiyo unayoisema. Kwa hivyo, tutaanza majaribio hayo, tunakwenda kisayansi, hii siyo blaa-blaa ya siasa mzee, tunakwenda kisayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunafanya majaribio tuone hasara na faida zake, tukijiridhisha kwamba ni kitu ambacho tunaweza tukakifanya ndiyo tuna launch sasa scale up project kwa nchi zima. Kwa hivyo, kwa mwaka huu tunafanya majaribio na ni hatua nzuri kwa sababu zamani tulikuwa hata tunaogopa kuruhusu watu kupimwa bila kuwa na ushauri nasaha kutoka kwa wataalam kwa kuepuka mambo mengine ambayo yangeweza kuibuka.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nataka kutoa ufafanuzi kwenye swali la nyongeza la Mheshimiwa Khadija Nassir kwamba tuna mikakati gani ya kuzuia maambukizi mapya. Kati ya mkakati mkubwa ambao tumeutekeleza na tunaendelea kutekeleza katika kupunguza maambukizi mapya ya VVU ni kupunguza maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili tumefanikiwa sana, asilimia 92 ya vituo vyetu vya huduma takribani 5,200 vinatoa huduma ya kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. Takribani wanawake zaidi ya asilimia 90 wote wanaohudhuria katika kliniki ambao ni wajawazito wameweza kupata huduma wale ambao wamekutwa na maambukizi. Tumefanikiwa sana Tanzania, kwa sababu ya mkakati huu, tumepunguza maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kutoka watoto 14,000 hadi watoto 6,500. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huo ndiyo mkakati mkubwa na niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge katika maeneo yetu, katika majimbo yetu, tuwahimize wanawake wajawazito mara tu wanapojigundua kwamba ni wajawazito waende kliniki lakini pia wapime UKIMWI kwa sababu wataweza kuzaa watoto ambao hawatakuwa na maambukizi ya UKIMWI. Niliona nilisisitize hili. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Niwatakie mfungo mwema ndugu zangu Waislam ndani ya Bunge na nchi nzima. Kwa wale ambao ni viongozi watumie Mwezi huu Mtukufu kujitathmini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii pamoja na sheria nyingine mbovu za habari, siyo tu zinabana wananchi kupata habari, bali zinatumika pia kufunga watu jela ovyo kisiasa. Mfano, mimi nilifungwa kwa kujadiliana na wananchi wangu taarifa za watu kupigwa risasi, watu kutekwa, maiti kuokotwa kwenye viroba, watu kutokuwa na uhuru wa kuongea na kadhalika…
Kitu ambacho siyo mimi tu niliyejadili, kwa sababu kilishajadiliwa ndani ya Bunge hili na pia Maaskofu wa Katoliki pamoja…
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali, ni lini sheria hizi zitafutwa ili kulinda Katiba ya nchi hususani Ibara ya 18? (Makofi). Maslahi mapana ya demokrasia nchini. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sugu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie nafasi hii nimkaribishe Mheshimiwa Sugu hapa kwenye Jumba, karibu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake linasema kwamba zipo sheria ambazo wakati mwingine zinatakiwa kutazamwa. Kama nilivyojibu kwenye swali la nyongeza lililotangulia ni kwamba sheria zote, siyo hiyo sheria moja, Serikali inayo mechanism ya kuzitazama wakati wowote. Kama kuna maeneo ambayo yanahitaji marekebisho au kuunganisha sheria au kuiondoa, ni Bunge hili linapata nafasi hiyo ya kufanya hivyo. Kwa hiyo, labda kama kuna eneo mahsusi Mheshimiwa Sugu kwa sababu umekuja, tuonane ili nami nipate kwa upana unachokizungumza, halafu baadaye sisi kama Serikali tutatazama kwa nia nzuri ya kuweza kufanya sheria iwe bora zaidi.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante, good to see you again. (Kicheko)
Mheshimiwa Spika, pamoja na matatizo waliyokuwa nayo polisi kwenye masuala ya vyombo vya usafiri lakini nikuhakikishie Jeshi la Magereza lina hali mbaya sana, siyo tu magari mabovu ni kwamba hawana magari kiasi kwamba wanafikia kupeleka wafungwa ambao wana kesi au rufaa wanawafunga pingu wanawapeleka Mahakamani kwa miguu. Sasa hii ni mbaya sana kwa usalama wao Askari Magereza, lakini pia kwa usalama wa wale watuhumiwa ambao wamefungwa pingu na kutembezwa kwa miguu kwa sababu mathalani mtu anatuhumiwa kwa ujambazi halafu anapita mitaani wale wanaomtuhumu wanamuona, wanaweza wakamvamia na kumshambulia na kuhatarisha maisha ya yule mfungwa. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Sugu kwa kuuliza swali kwa experience na niseme tu kwamba yeye ni mshauri mzuri tutazingatia hilo ili tuweze kuweka mgao upande Jeshi la Magereza ili kuweza kuepuka tahadhari hiyo aliyoisema. (Makofi)
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ukiacha waaguzi lakini pia wafanyakazi wengi wa Idara zingine Serikalini wanacheleweshewa sana mafao. Mfano ni Askari Magereza wanastaafu lakini wanakaa zaidi ya miaka miwili hawajaenda kwao. Wanaganda kwenye zile kota za Magereza lane, mafao hamna, mtu kastaafu miaka miwili anadhalilika kwao Tanga, kwao Kilimanjaro, kwao wapi, hawezi kwenda kwa sababu hajapewa mafao yao wala pensheni.
Mheshimiwa Spika, sasa hii Serikali inawaangalia kwa jicho lipi hawa Askari Magereza kwa sababu, wao wamezoea kuwa-support Polisi ambao wanatukamata, lakini wahalifu wako maeneo mbalimbali, wanakusanywa yale maeneo mbalimbali, wanapelekwa eneo moja ambalo ni Magereza. Wale jamaa wana kazi ngumu sana kuwatunza mle, lakini wanafanya utumishi wao, wanakuja wanastaafu, mtu anakaa Police Lane miaka miwili hajapewa pension wala mafao yake, kwa nini wanawafanyia hivi Askari Magereza? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ameuliza, kuhusu mkakati wa Serikali yetu, naomba nimwambie Mheshimiwa Mbilinyi, mkakati wa kwanza wa Serikali yetu ilikuwa ni kulipa madeni yote ya michango ya mwajiri ambayo Serikali ilikuwa ikidaiwa na mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Napenda kumwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba, mpaka leo ninapoongea madeni yote yaliyokuwa yanadaiwa ya michango Serikali yetu ya Awamu ya Tano tayari imeshalipa zaidi ya shilingi bilioni 282 ili kuhakikisha wastaafu wetu wanalipwa mafao yao kwa muda muafaka.
Mheshimiwa Spika, mkakati wa pili, ilikuwa ni kuona jinsi gani ya kuunganisha Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii, ili pesa zilizopo ziweze kutumika inavyotakiwa na kuwanufaisha wastaafu wetu pale wanapostaafu. Namwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba, Julai Mosi, mifuko yote imeshaunganishwa na sasa tuna mifuko miwili, tatizo hili litaondoka bila wasiwasi wowote.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ili kuondoa ile dhana kwamba hatupongezi kila kitu, naomba niseme kwamba naipongeza Wizara na hasa Katibu Mkuu aliyepita Dkt. Mpoki, kwa kutoa ushirikiano kwa Mbunge katika hili mpaka hapo tulipofika na jengo kukamilika na CT-Scan kupatikana. Swali la kwanza, ningependa kujua sasa, hiyo MRI chini ya huo Mradi wa ORIO itafika lini ili jengo lile lianze kazi? Kwa sababu tunalifuatilia na kwa taarifa tulizonazo ndani ya wiki mbili litaanza kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, vipi kuhusu wataalam (specialists), maana tunafanikiwa kwenye majengo ila mara nyingi tunakuwa na uhaba mkubwa wa specialists. Binafsi, kama ningeweza kumshauri Mheshimiwa Rais, ningemshauri huyu Dkt. Mpoki aliyekuwa Katibu Mkuu kuliko kupelekwa Ubalozini angeletwa hata kuwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya kwa sababu ule utaalam wake ni muhimu sana kwa Taifa na wako Madaktari wachache sana wenye utaalam ule. Kwa hiyo, kumpeleka mbali, ni kupeleka huduma mbali kutoka kwa Taifa. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa kwa kuipongeza Serikali, nami nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufanya ufuatiliaji wa karibu katika suala hili la ujenzi wa jengo la radiolojia katika Hospitali ya Rufaa ya Mbeya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na ni lini Serikali itapeleka mashine ya MRI; kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, ni kwamba sasa hivi Serikali kupitia Mradi wa ORIO ambao tunashirikiana na Serikali ya Uholanzi, ina kusudio la kupeleka mashine za radiolojia kwa maana ya X-Ray, Digital X-Ray, mashine za fluoroscopy, CT-Scan pamoja na MRI. Kwa hiyo, mchakato huo unaendelea. Tunategemea katikati au mwishoni mwa mwaka huu, utaratibu huo utakuwa umekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake la pili, Madaktari bingwa katika eneo hili; mkakati ambao tunakwenda nao sisi kama Wizara kwa sasa hususan katika wataalam wa Sekta ya Radiolojia, tumeamua kwamba tutumie ubunifu na teknolojia ya kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyoongea, huko duniani X-Rays zinazopigwa mathalan katika nchi ya Marekani, nyingine hazisomwi Marekani, zinasomwa katika nchi nyingine kwa kutumia teknolojia. Hizi mashine za Digital X-Ray ambazo tunazifunga sasa hivi, sisi kama Wizara tumeamua kuweka kituo chetu pale katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ambapo tutaunganisha na mtandao wa fibre- optic, kutakuwa na screen pale ili picha ambazo zitakuwa zinapigwa Tanzania nzima kwa teknolojia hii, ndani ya dakika tano picha umepata. Tunaweza tukatuma kwa njia ya mtandao, zitasomwa Dar es Salaam na majibu ndani ya dakika 15 kurudishwa katika eneo husika. Kwa hiyo, tumejipanga vizuri sana katika eneo hilo.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru niko kwenye runway, ningependa kujua kwa Mheshimiwa Waziri ni lini ujenzi wa jengo la abiria pamoja na taa kwenye njia za kurukia yaani runway zitakamilika kwenye uwanja wa ndege wa Songwe Mbeya ili uwanja ule uweze kufikia full capacity?

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sasa hivi hata kukiwa na ukungu tu kidogo kwa sababu hakuna taa na unajua ndege nyingi pilot hawezi kutua kama haoni umbali wa futi 700 kutoka juu kwenda uwanja wa ndege kama haoni hawezi kutua. Sasa kukiwa na ukungu kidogo ndege haitui, mwenyewe nimesharudi Dar es Salaam mara mbili na ndege kwa kushindwa kutua mchana kabisa kwa sababu ya ukungu na tatizo kubwa likiwa ni taa za kwenye runway.

Sasa ningependa kujua lini vitu hivi vitakamilika jengo la abiria pamoja na taa ili Songwe International Airport iwe full capacity?
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Mbunge kuhusiana na kukamilisha mradi wa ujenzi wa Kiwanja cha Songwe ni kwamba tunatangaza tender mwezi huu, mwezi wa tatu tutakuwa tumeshampata mkandarasi na kukamilisha runway kutachukua miezi miwili. Baada ya hapo sasa tutaenda kwa ajili ya tender ya kukamilisha jengo. Kwa hiyo, usiwe na wasiwasi kiwanja cha Songwe ni katika viwanja vikubwa kikiwepo cha Julius Nyerere kiwanja cha Mwanza na KIA. Kwa hiyo, malengo ya Serikali ni kuhakikisha viwanja vyote hivyo vinaboreshwa na kufanya dreamliner iweze kuruka viwanja vyote.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini tunakubaliana kwamba masuala ya utafiti kwa ujumla nchini yamedorora sana. Hii ni kwa sababu vituo vya utafiti kikiwemo Kituo cha Utafiti Uyole - Mbeya viko hoi. Uyole iko hoi kimiundombinu na hata kibajeti. Sasa ni lini Serikali itatambua umuhimu wa vituo hivi kama zamani ili kuvipelekea bajeti stahiki tupate kuboresha kilimo nchini na hasa kituo cha Uyole Jijini Mbeya . Miundombinu iko hovyo, hata hali za wafanyakazi ziko hovyo. Before wakati tuko…

NAIBU SPIKA: Umeshauliza swali Mheshimiwa. Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo, majibu kwa swali hilo.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbilinyi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze kwa ajili ya kuviona vituo hivyo, lakini nataka nimhakikishie kwamba, kama Serikali hatujawahi kuviacha nyuma vituo hivi kama anavyodai na ndiyo maana mwaka juzi 2017, tulileta Muswada wa Sheria na Bunge hili likaridhia. Kwa ajili ya kuviboresha vituo vile, tuliweza kuunda Sheria maalum ile Sheria hatari na kuunda vituo vyetu nane vikuu na nane vidogo, jumla vituo 16 na kuvipangia majukumu mahususi kwa kila kituo mazao mawili mawili ili kuyapunguzia mzigo.

Mheshimiwa Naibu Spika, yote haya ni katika kuweka juhudi za msingi ili vituo hivi viwe na mazao machache ya ku-focus badala ya kubeba mazao yote na sasa hivi tuko kwenye mchakato wa bajeti na miongoni mwa vipaumbele tulivyovipa na katika hivi vituo vya utafiti kwenda kuviongezea uwezo pia kuviboresha miundombinu yake ili viweze kukidhi matarajio ya wakulima wa nchi hii.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Tatizo la maji la Jiji la Dar es Salaam linafanana kabisa na tatizo la maji la Jiji la Mbeya. Katika Jiji la Mbeya, wataalam wameshasema, solution ya tatizo ni kutoa maji kutoka mto Kiwira, feasibility study imeshafanyika, taarifa tunazo na mto Kiwira hauko mbali, ni kilomita chache sana kutoka Mbeya. Naamini Mheshimiwa Waziri anajua hata bajeti inayotakiwa kutokana na ile feasibility study.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lini fedha itapelekwa katika ile project ili ile project ifanyike tuondoe tatizo la maji kwenye maeneo ya Uyole, Mwakibete na hususan maeneo kama Shewa ambako wananchi wanapata taabu sana na wako Jijini, wanalipa kodi za Jiji.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge wa Jiji la Mbeya, kaka yangu Sugu, amezungumza suala la msingi sana. Kweli tunatambua kabisa katika suala zima la maji katika Jiji la Mbeya kumekuwa na ongezeko kubwa sana la watu, lakini tunaona kabisa tukiyatoa maji mto Kiwira na kuyaleta tutakuwa tumetatua kabisa tatizo la maji. Nataka nimhakikishie kwamba utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Maji tumejipanga katika kuhakikisha kupitia mapato yetu ya ndani lakini pia kwa wafadhili mbalimbali tupate fedha ili tuwekeze na wananchi wa Mbeya waondokane na tatizo hili la maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwenye barabara kuu ya Dar es Salaam - Morogoro tumeona sasa hivi wamefunga cameras. Sasa kwa nini camera zile zisifungwe nchi nzima ili sasa baada ya kufungwa zile camera Askari wanaokaa barabarani warudi vituoni, waende wakashughulike na masuala mengine ya wahalifu, kwa sababu msingi wao wa kukaa barabarani mkubwa ni speed. Sasa kwa kuwa zinafungwa camera ambazo zitakuwa zinachukua picha, zinatuma report kwenye database, wherever halafu zile report zinafuatiliwa hata baada ya wiki mbili, mwezi mmoja mtu anapelekea tiketi kwa mujibu wa details za gari lake. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMB0 YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, huu ndiyo mwelekeo wa Serikali yetu. Ni imani yetu kwamba, mambo yatakapokuwa yamekaa vizuri kibajeti tutafunga camera katika Miji mikuu yote na maeneo mengine nchi nzima. Kwa hiyo ni suala tu la kuvuta subira na kazi hiyo itafanyika hatua kwa hatua kadri ya hali ya fedha itakapokuwa inaruhusu.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kama lilivyo tatizo la maji katika Jimbo la
Momba kwenye Jiji la Mbeya sasa hivi tatizo la maji tunaweza tukasema ni janga. Bonde lote la Uyole maji ni tatizo, ni kukavu kabisa, wananchi wanyonge wananunua maji mpaka ndoo Sh.500, maisha haya yalivyokuwa magumu. Maeneo ya Mwakibete na Ilomba, kote maji ni tatizo. Tumeshauri ili kutatua tatizo la maji Mbeya tutoe maji Mto Kiwira iwe kama source.

Mheshimiwa Spika, cha ajabu akija Rais au Waziri Mkuu maji Mbeya yanatoka, hayakatiki, wakiondoka maji yanakatika. Tatizo nini hasa ambalo linafanya changamoto hii ya maji katika jiji la Mbeya lisitatulike wakati vyanzo vya maji tunavyo na miundombinu ipo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kumjibu kaka yangu Mheshimiwa Mbilinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo nataka kusema ni kwamba Jiji la Mbeya sasa hivi limekuwa na ongezeko kubwa sana la watu. Kwa hiyo, mahitaji na uzalishaji wetu umezidiwa kutoka na ongezeko kubwa la watu.

Mheshimiwa Spika, mimi kama Naibu Waziri wa Maji nilifika Mbeya na nimejionea hali halisi na kweli nimefika katika chanzo cha Mto Kiwira tumeona hiki ni chanzo pekee ambacho kinaweza kikatumika na kutatua tatizo la maji la Mbeya. Tumekubaliana sisi kama Wizara kuangalia namna ya kufanya usanifu ili sasa tuweze kutumia chanzo cha Mto Kiwira katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji katika Jiji la Mbeya.

Mheshimiwa Spika, lakini haki ya mwananchi ni kupatiwa huduma ya maji. Niwaagize Wakurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira ya Mbeya kuhakikisha inatoa huduma hii maji, kwa uchache wake, lakini kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma muhimu na bora si mpaka kiongozi aweze kufika. Cha msingi nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara tumejipanga kuhakikisha tunatatua tatizo hili la maji katika Jiji la Mbeya.