Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Atupele Fredy Mwakibete (33 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa wingi wa rehema kwa jinsi ambavyo alituchagulia viongozi kwa ngazi zote; nikianza na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Joseph Pombe Magufuli; Makamu wa Rais, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu; na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa.
Pili, napenda kuchangia kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Busokelo ni Jimbo ambalo tunalima mazao ya chakula na mazao ya biashara. Mazao ya chakula tunayolima ni kama yafuatayo: ndizi, mahindi, maharage, viazi mviringo na viazi vitamu, matunda mbalimbali kama maparachichi, matunda damu na mengineyo. Mazao ya biashara ni kama yafuatayo: mbao, chai, kokoa, kahawa pamoja na hiliki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mazao hayo yote, hatuna hata kiwanda kimoja kwa ajili ya kuchakata mazao hayo yote. Inasikitisha sana kuona mkulima, tena wa jembe la mkono analima kwa taabu sana, pembejeo haziwafikii kwa wakati, zinakuja wakati muda usiofaa. Kwa mfano, mbolea za kupandia zinakuja wakati wa kupalilia na mbolea za kukuzia zinamfikia mkulima wakati anavuna. Mbaya zaidi mkulima huyu akifanikiwa kuvuna,hapati sehemu za kwenda kuuza ama kuchakata (viwanda vidogo) ili mazao yao yapate thamani kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri awakumbuke wananchi hawa wa Busokelo kwa kututafutia wawekezaji wa mazao kama kokoa, ndizi na mahindi pamoja na viwanda vya mazao ya ng‟ombe mfano, maziwa (kiwanda cha maziwa) Kata ya Bonde la Mwakaleli (Isange, Kandete, Lubeta na Mpembo).
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atusaidie kutafuta wawekezaji kwenye viwanda vya gesi aina ya cabondioxide gase Co2, pamoja na umeme wa joto ardhi Geothermal eneo la Ntaba, Kata ya Ntaba ndani ya Busokelo Mkoani Mbeya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana tuwe na kiwanda cha kusindika kokoa kwa sababu wakulima hawa wanalima kwa wingi sana hasa maeneo ya lufilyo, Ntaba na Kambasegela ili thamani ya kokoa ipande na mkulima aweze kupata zaidi kuliko hivi sasa na itaongeza morali zaidi kwa wakulima wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu ya Jimbo la Busokelo ni mibaya sana hasa kipindi hiki cha mvua na hivyo imepelekea zaidi ya tani nyingi sana za ndizi na maparachichi kuharibika na hivyo kusababisha umasikini zaidi kwa wakulima hawa. Namwomba Mheshimiwa Waziri, ni muhimu sana viwanda hivi vikajengwa maeneo husika ili hasara ambayo inatokana na kuharibika kwa miundombinu iweze kuepukika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchangia hayo hapo juu, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Mheshimiwa Spika, lakini kabla sijaanza kuchangia, napenda kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa sababu tangu uchaguzi umefanyika ametuteulia viongozi na tumepata jembe, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Pia napenda kukishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa jinsi ambavyo mmekuwa nami tangu kipindi chote cha uchaguzi na hadi sasa tumepata nafasi ya kuingia Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mimi nasema afya kwanza kwa sababu hakuna Mbunge au mwananchi yeyote ambaye anaweza akafanya shughuli za maendeleo pasipokuwa na afya. Katika kampeni zangu nilikuwa nasema afya kwanza na leo hii ikibidi naomba iwe slogan ya Taifa kama Mheshimiwa Waziri atakubaliana nayo. Napenda kuwashukuru Mawaziri kwa kazi nzuri mnazozifanya pamoja na Naibu Mawaziri kwa jinsi ambavyo mnajituma na kwa kweli hakika hapa kazi tu, tunaiona hii kazi inafanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, bahati nzuri nimekuwa katika sekta hii ya afya kwa kufanya kazi na mashirika ya watu wa Marekani kupitia Jeshi la Amerika. Kwa hiyo, nafikiri Mheshimiwa Waziri ataweza kupata ushauri wangu katika mambo mbalimbali. Nikianza kwanza na Jimbo langu la Busokelo. Busokelo ni Jimbo ama ni halmashauri mpya ambapo hadi sasa ninavyosema tuna watumishi wanne tu ambao ni specialist, kwa maana ya wanaume wawili na wanawake wawili. Ni sawa na kusema asilimia 100 hatuna watumishi kwa mujibu wa takwimu za kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 140.
Mheshimiwa Spika, lakini pia katika Halmashauri ya Busokelo, tuna kituo kimoja tu cha afya kwa maana ya kata 13, kituo kimoja. Najua hili lipo chini ya TAMISEMI lakini kwa sababu hizi ni Wizara ambazo zina mahusiano, napenda pia Mheshimiwa Waziri alifahamu hili. Pia hatuna hata hospitali ya wilaya tunatumia Hospitali ya Kanisa inaitwa CDH. Eneo tumeshaliandaa na tumeshaanza harakati lakini tunaomba pindi tutakapoomba msaada kutoka Serikalini muweze kutukumbuka katika hili.
Mheshimiwa Spika, siyo hilo tu katika Kituo cha Afya cha Kandete ambacho ndicho kituo pekee, kinahudumia wananchi wengi sana kwa maana ya Bonde zima la Mwakaleli. Ukianzia na Kata za Itete, Kandete yenyewe, Isange, Mpombo mpaka Wangwa. Huduma zinazotolewa pale ni ambazo hakika, kama hujapata huduma pale maana yake inabidi usafiri umbali wa zaidi ya kilometa 50 kufuata huduma hizo mjini ambako ni Tukuyu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba kituo hiki kiwezeshwe tukianzia na masuala ya mochwari hatuna na hata dawa nazo zinafika kwa kusuasua sana. Kwa mfano MSD wamepewa jukumu la kusambaza ama kusimamia tunasema Medical Store Department nchi nzima. Wakati mwingine MSD wanachokifanya utashangaa imebaki kama mwezi mmoja, ama miezi miwili kusambaza hizo dawa kwa maana zinakuwa expired lakini wanazisambaza. Kwa hiyo, zinakuwa hazina manufaa kwa wale wanaopelekewa kwa sababu kipindi kifupi tu zinakuwa tayari haziwezi tena kutumika kwa afya ya binadamu.
Mheshimiwa Spika, nizungumzie sasa suala la huduma za UKIMWI katika nchi yetu ya Tanzania. UKIMWI ni janga la Kitaifa na Kimataifa na kwa bahati mbaya sana bajeti ya Serikali imekuwa kidogo sana ukilinganisha na uhitaji wa huduma kwa ugonjwa huu wa UKIMWI. Kuna mashirika mawili hapa nchini, kuna Global Fund na PEPFAR. PEPFAR ni President’s Emergency Plan For AIDS Relief, ni shirika ambalo liko chini ya Serikali ya Marekani, lilianzishwa enzi za Rais, Mheshimiwa Bush. Pamoja na kwamba tunatumia Global Fund ambayo ni nchi mbalimbali lakini asilimia kubwa bado inachangiwa na Serikali ya Marekani.
Mheshimiwa Spika,In case imetokea hawa Wamarekani wanasema sasa stop kuchangia Afrika na Mataifa mengine hakika Tanzania hatutakuwa sehemu nzuri. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali kupitia Wizara hii waongeze bajeti ya kutosha katika masuala ya UKIMWI. Wakati mwingine wengi wetu tunaonesha kidole kimoja hivi kwamba yule yule ndiye anaishi na HIV lakini kwa tafiti ambazo tumefanya kwa miaka yote, kumbuka vidole vitatu vinakuonesha wewe.
Mheshimiwa Spika, niwape mfano mmoja, nilipokuwa nasimamia Nyanda za Juu Kusini, Mikoa ya Ruvuma, Katavi, Rukwa, Mbeya, nililia sana nilipofika Hospitali ya Rukwa Mjini, nilimkuta bibi mmoja kizee sana ni mgonjwa, anasema mjukuu wangu hapa sina hata Sh.1,000 ya kununua dawa. Sasa umepataje huu ugonjwa? Anasema nilikuwa namlea mjukuu wangu na kwa sababu hatuna elimu ya kumtunza mtu wa aina hiyo ndiyo nikaupata maana alikuwa hatumii hata gloves. Hakika ilikuwa ni masikitiko makubwa, hata Sh.1,000 za kununua dawa hana. Kuna dawa kwa ajili ya kuzuia opportunistic infections, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla atakuwa anafahamu, Serikali haitoi hata wafadhili pia wamejitoa.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, lazima kama Serikali tutie nguvu sana kwa upande huo kwa sababu dawa hizi za opportunistic infections zinazuia mambo mengi. Kuna zile ambazo zinazuia fungus, magonjwa ya ngozi na vitu vingi ukiachana na zile tunazoita TLE (Tenofovir/Lamivudine/Efavirenz) ambazo hizo zinatumika hasa hasa kwa upande wa matibabu kwa mama mjamzito na anayenyonyesha. Kwa hiyo, kwa sababu wafadhili nao wanajitoa kuleta hizi dawa za opportunistic infections, ni vizuri sasa tutenge bajeti ya kutosha ili kuzuia maradhi ambayo nimeyatamka hapo awali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba pia nichangie kidogo katika suala la Hospitali ya Rufaa Mbeya. Hospitali hii inahudumia Kanda nzima, iwe Njombe, Iringa, Rukwa, Ruvuma, Katavi watu wanakwenda kutibiwa pale. Kipindi kile wakati inajengwa ilikuwa ni watu milioni mbili, lakini sasa ni zaidi ya watu milioni nane. Kwa hiyo, tunaomba Serikali hata kupitia Wizara ya TAMISEMI tuweze ku-expand ili iweze sasa kuendana na mahitaji ya sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, si hivyo tu hata Wabunge wenzangu wamezungumzia masuala la CT-Scan, hawana CT-Scan pale na hiyo ndiyo hospitali ya rufaa. Kama hakuna CT-Scan tusitegemee watu wale wanaweza wakapata huduma zilizo bora na sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, naomba nizungumzie suala la TEHAMA, mimi pia ni mtaalam wa mambo ya TEHAMA. Leo hii tunazungumzia ulimwengu wa sayansi na teknolojia ni lazima tuhusishe pia Wizara ya Afya. Mtu kutibiwa popote pale alipo. Tunazungumzia suala la uhaba wa Madaktari Bingwa lakini kuna solution ama majawabu ambayo yanaweza yakatusaidia kama tutaweza ku-adopt, inawezekana isiwe leo au kesho lakini tuwe na wazo kwamba kuna kitu hiki kinafanyika duniani na Mataifa mengine yaliyoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna kitu kinaitwa Telemedicine. Telemedicine ni suala la kutibu mgonjwa popote pale alipo. Kwa maana ya kwamba unaweza ukafanya naye appointment lakini utafanya baada ya kumsaidia kwa kutumia hata hizi simu za mkononi, wengi wetu tunatumia tu WhatsApp, Facebook na vitu vingine lakini simu inaweza ikafanya vitu vingi zaidi ya hivi. Kwa hiyo, Wizara naomba ilichukue wazo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pia nimeshiriki sana kuandaa na kufanya analysis za Wizara kwa maana ya kutumia tools zinaitwa database, C2C database, DHIS - District Health Information System, LAS - Lap Assessment Response System. Hizi database ni nzuri sana kwa maana ya kwamba inaweza ikaunganisha nchi nzima kufanya analysis ya tuko wapi, ni mkoa gani unaongoza na tufanye nini kwa ajili ya intervention zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninachoiomba Wizara ni kwamba, inabidi hizi system ziwe integrated. Kwa mfano, C2C database ina version nyingi sana lakini ni muhimu sasa iwe ni web-based sasa hivi ni stand-alone, nikisema stand-alone najua mnafahamu nyie Madaktari hasa wale wataalam wa Wizara kwa maana ya kwamba ukipeleka kituoni iko pale pale inabidi tena uhamishe kwa njia ya flash ama external kuipeleka sehemu nyingine. Pamoja na hayo hii LAS - Lapla Response System imekuwa na combined na Post Training Follow-up na itasaidia sana kwa maana ya ngazi ya Wilaya. Kwa ngazi ya Wilaya itakuwa inatuma ripoti moja kwa moja kwa Wizara na haya ndiyo maboresho katika sekta ya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kabla sijamaliza naomba nizungumzie suala la huduma kwa mtoto, maambukizi ya virusi vya UKIMWI (VVU) kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. Kwenye hotuba ya Waziri, ukurasa wa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana katika uchumi wa nchi yetu, Wizara ya Nishati na Madini. Nakushukuru wewe kwa kazi nzuri unayoifanya, pia nimshukuru Mungu kwa kutupa nafasi hata kufika mahali hapa siku ya leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mungu zaidi kwa jinsi ambavyo alimwongoza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kumchagua Profesa Sopeter Muhongo katika Wizara hii ya Nishati na Madini. Profesa hakika unaitendea haki sana Wizara hii. Pia niwashukuru wale wote ambao ni Watendaji Wakuu, Katibu Mkuu, Mkurugenzi wa REA Tanzania, Dkt. Lutengano Mwakahesya, Mkurugenzi wa Geothermal Tanzania na Watendaji wengine wote katika nishati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya shukrani hizo mchango wangu nielekeze zaidi nikianza na umeme wa vijijini (REA). Mpango huu wa umeme vijijini hakika mwaka jana wengi wetu tumeokoka sana katika mpango huu wa REA. Tumeokoka kwa sababu pamoja na kwamba siyo vijiji vyote vimepata, naamini katika awamu hii ya III vijiji vingi vitapata umeme huu. Nikija katika Jimbo langu la Busokelo, Busokelo ni miongoni mwa Majimbo ambayo tumenufaika na mpango mzima wa REA. Pamoja na kwamba kuna changamoto za hapa na pale, kuna baadhi ya maeneo kama Lupata, ukienda Isoko, ukienda Mpata, ukienda na maeneo mengine ya Kilimansanga bado umeme huu haujafika lakini tuna imani kwamba vijiji 30 vilivyosalia, tunaamini katika mpango huu wa awamu ya III vitapata umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala zima la mpango wa umeme vijijini, kwa vile vijiji ambavyo vilikuwa awamu ya pili, tunaomba watendaji pamoja na wahusika wote vikamilike kabla ya Juni ili wananchi wale kwa sababu tulishawaaminisha kwamba watapata umeme, na walituamini, tunaomba kabla ya Juni kwisha waweze kupatiwa huo umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la madini. Mkoa wa Mbeya ni miongoni mwa mikoa ambayo imebarikiwa sana katika nchi yetu ya Tanzania. Tuna madini ya aina nyingi sana, ukienda kule Chunya utakuta kuna gold, ukienda huku Ileje utakuta kuna madini, ukienda Kyela makaa ya mawe, ukija Busokelo, kwa hiyo tuna madini ya aina mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na madini aina ya calcium yanayopatikana pale Mlima wa Panda Hill. Mheshimiwa Waziri katika kitabu chake haya madini sijayaona hapa, lakini naamini kwamba atatuma timu yake waweze kufanya exploration na extraction kule, basi wananchi wale watafaidi sana haya madini kwa sababu tunaamini hata utengenezaji wa mbolea aina ya NPK inatokana na madini hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, nikisoma kitabu cha hotuba na Waziri ameandika vizuri sana, very technical, ukurasa wa 62 kuna madini aina ya niobium, madini haya pia Mbeya yanapatikana na kazi kubwa ni kutengeneza vifaa vya elektroniki ikiwemo pamoja na engine za ndege tunaita jet, lakini pamoja na kutengenezea vitu mbalimbali, mambo kama kompyuta na simu. Kwa hiyo, tunaomba kama yataweza kuendelezwa, pamoja na kwamba upembuzi yakinifu ulishafanyika na utafiti umefanyika, sasa kazi kubwa iliyobaki ni kwamba yaanze kufanyiwa kazi kwa maana ya kuchimbwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujumuisha hotuba yake hapa atuambie kwamba ni lini hasa rasmi wananchi wa Mbeya, katika maeneo ya Panda Hill, Mbeya na Tanzania kwa ujumla watanufaika na haya madini ili waweze kuinua uchumi wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikija katika suala la geothermal (jotoardhi). Geothermal ni umeme ambao unatokana na nguvu ama joto lililoko ardhini na Busokelo tumebahatika kuwa na sehemu inayopatikana hiyo geothermal. Kwa hiyo naomba nimshukuru Waziri kwanza kwa sababu nakumbuka siku ile alikuja, alifika katika eneo hili la Mto Mbaka na alituahidi kwamba mara tu baada ya uchunguzi ama baada ya utafiti kukamilika mwezi wa Septemba wataanza kuchoronga visima vya huko, kwa hiyo tunaomba asitusahau.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwomba pamoja na timu yake ya wataalam waje katika eneo hili kwa sababu wananchi wakati tunahimiza kwamba wasifanye maendeleo yoyote kwa sababu hili eneo litakuwa ni sehemu mojawapo ya kuzalisha umeme na sisi tutakuwa tunauza maeneo mengine, walisikiliza ile kauli kwa sasa hivi wanasubiria.
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo geothermal pekee tu, katika Jimbo la Busokelo pia tuna gesi aina ya carbondioxide. Hii gesi imeanza kuchimbwa tangu mwaka 1984, lakini kwa bahati mbaya hata hivi sasa ninavyoongea tuna viwanda viwili, kimoja kipo Kanyelele na hii gesi inatoka Kijiji cha Mpata, lakini pia kuna kiwanda kingine karibu na Tukuyu Mjini kwa ajili ya gesi hii na gesi hii inatumika zaidi katika masuala mazima ya kwenye soda, kwenye bia na maeneo mengine ambayo yanasababisha vitu visioze wala visiharibike.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bahati mbaya, kwa makampuni ambayo yamewekeza kule, kuna kitu tunaita social responsibility kwa maana ya jamii inayozunguka, huwa hawafaidiki na gesi hii. Tunaomba Mheshimiwa Waziri, kwa nguvu zako zote pamoja na watendaji wako wote kuisimamia vizuri gesi hii aina ya carbondioxide kwa sababu wananchi wanaona yanakwenda magari na kurudi kuchukua, lakini hawaoni wananufaikaje na hii gesi. Hii ni changamoto kubwa sana, kwa sababu nakumbuka kipindi tunaomba kura ni miongoni mwa mambo ambayo yalitusababisha tupate wakati mgumu sana. Kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri alizingatie hilo atakapokuwa anajumuisha hotuba yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na suala hilo, ukienda Kata ya Lufilyo kuna madini ambayo yanapatikana kule kwa ajili ya kutengenezea marumaru na ukiangalia Tanzania nzima hii, mara nyingi sana tuna-rely kwenye marumaru za ku-import kutoka China lakini kule kuna madini ya kufanya hivyo. Katika Kijiji hiki cha Kikuba, Kata ya Lufilyo, kuna maji ama maporomoko ambayo yanaweza yakasababisha umeme wa Hydro Electric Power kwa maana ya umeme wa maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo basi, tunaomba wataalam ama watafiti waanze kuja kuchungulia kule kwa ajili ya kuleta wataalam ili waweze kutuambia ni kitu gani pengine baada ya hapo kitafuata ili wale wananchi wasiangalie tu yale maji yanakwisha pasipo faida yoyote, naamini tukiwekeza katika umeme itatusaidia sana kama nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala zima la matumizi ya umeme. Mara nyingi sana tunasema umeme; naishauri Serikali tuanze kutoa elimu kwa jamii kwamba umeme huu siyo kwa ajili ya kuwasha taa, siyo kwa ajili ya kupiga pasi tu, siyo kwa ajili ya kuangalia TV ama runinga, tufikiri katika uwanja mpana hasa kwa maana ya kuleta viwanda vidogovidogo, vile vya kuchakata hata kwa mikono yao. Nafikiri umeme utakuwa na faida sana na REA hii itakuwa na faida sana kwa wananchi kama tutaanza kutoa elimu ya namna hiyo. Maana wengi wetu wanafikiri kwamba umeme ni kwa ajili ya kuwasha taa na pengine kuangalia vitu vingine, lakini kumbe umeme ni zaidi ya matumizi hayo. Nafikiri elimu hii ikiwafikia na kama Wizara watakuwa na mipango ya kutoa elimu hiyo kwa jamii itapendeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nizungumzie suala zima la Serikali kuhusika asilimia mia moja katika kuwekeza kwa maana ya nishati ya umeme. Umeme ni gharama kubwa sana, tunaomba Serikali kwa jinsi ambavyo wameshaanza kutafuta wadau wengine waendelee hivyo hivyo. Hakuna Taifa lolote duniani ambalo kwa nguvu zao wenyewe wanaweza wakajitosheleza katika nishati.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bahati nzuri nilipata nafasi ya kutembea Mataifa mengine duniani, kama Ujerumani, utakuta nyumba moja ya familia moja inakuwa na vyanzo vitano vya nishati ya umeme; utakuta kuna maji, utakuta kuna solar, utakuta kuna umeme wa upepo utakuta kuna umeme wa biogas, geothermal na kadhalika, hata ukikatika umeme wa aina moja, basi umeme wa aina nyingine ule una-take up, hivyo katika nchi yetu pia tuanze kufikiri katika mfumo huo, tusi-rely tu katika vyanzo vya umeme wa aina moja, kwa maana kwamba kuna gesi halafu pia kuna umeme wa maji, lakini pia tuanze kufikiri zile energy ambazo ni renewable kwa maana ya kwa mfano geothermal.
Mheshimiwa Naibu Spika, geothermal is an energy ambayo inakuwa renewable, inaweza ikazalisha umeme na kuzalisha na kuzalisha, lakini tuki-rely katika umeme wa maji, sisi wote ni mashahidi hapa, kwa sababu wakati mwingine, kama kipindi cha miaka miwili iliyopita nchi yetu ilikuwa katika janga kubwa, kwa hiyo umeme ama mabwawa ambayo tunategemea yalikuwa hayatoi maji sawasawa kama vile ambavyo tulitegemea. Pia tukija katika gesi, gesi ile ukisha-extract hatutegemei tena kwamba itaendelea kuwepo vilevile kwa miaka na miaka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niunge mkono Wizara hii na hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha aniambie ni lini umeme wa joto ardhi (geothermal) utaanza kuchimbwa uliopo Kata ya Ntaba. Je, wananchi wa maeneo hayo watanufaikaje na mradi huo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vijiji ambavyo vilikuwa kwenye awamu ya pili ya REA ila hadi sasa vijiji hivyo havijapata umeme. Tunaomba vijiji hivyo vipate umeme vilivyopo ndani ya Jimbo la Busokelo visivyopungua 30.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atusaidie migogoro ya ardhi iliyopo, moja kwenye Bonde la Mwakaleli kati ya TANAPA na wananchi wa Bonde la Mwakaleli katika Kata za Kandete, Luteba na Isange. Tunaomba irudishwe mipaka ya zamani ili wananchi hawa wapate nafasi za kufuga na kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wa Kyeruku uliopo Kata ya Kisegese, Kijiji cha Ngeleka, kwa sababu shamba hili wananchi wanalihitaji kulilima ili wajikomboe kwenye umaskini na kwa sasa shamba hili lipo tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Busokelo tumetenga maeneo tayari kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za NHC, wananchi hawa wapo tayari kununua nyumba hizo.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kushiriki kuchangia maoni yangu juu ya Mpango. Kabla kuanza kuchangia kwanza, nimshukuru Mwenyezi Mungu lakini pia niwapongeze Mawaziri wote walioteuliwa na zaidi nimpongeze Mheshimiwa Mpango na Naibu wako pamoja na watendaji wote katika Wizara hii ya Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Mpango wetu ukianza na ule ukurasa wa 34 hasahasa katika suala la afya imeonesha kwamba utajikita zaidi katika kuboresha Hospitali za Kanda na Mikoa mbalimbali. Mimi nataka niongezee jambo moja kwamba katika Sera ya Afya kama ambavyo tunajua wote inatakiwa kila kijiji kiwe na zahanati, kila kata iwe na kituo cha afya na kila Wilaya iwe na hospitali. Kwa mantiki hiyo katika huu ukurasa wa 34 sijaona kama haya mmeyazingatia kufuatana na Sera ya Afya ambavyo inataka. Kwa hiyo, ningependa hili jambo mlizingatie mtakapokuwa mnaleta ile final draft.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili katika jambo hilo hilo ni katika suala la matibabu (telemedicine). Nimeona mmekazia sana kupeleka ama kutibu watu ambao tayari wameshaathirika na magojwa mbalimbali, aidha, iwe nyemelezi ama yawe magojwa yale ya kuambukiza. Kwa hiyo, nilitaka nitoe maoni yangu kwamba ni muhimu sasa kutoa elimu kwa jamii kuhusu magonjwa mbalimbali kabla ya kuanza kuyatibu kwa sababu tunasema prevention is better than cure kwa maana nyingine ni kheri kinga kuliko tiba na ndiyo maana Serikali inatumia pesa nyingi sana kutibu wakati pengine tungetumia fedha nyingi zaidi kutoa elimu kwa hayo magojwa nafikiri kizazi chetu cha Tanzania tungekuwa tuko salama zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependekeza kwamba muongeze neno ama teknolojia ya kutibu kwa njia ya mtandao (telemedicine). Hii teknolojia nimekuwa nikizungumza humu Bungeni tangu mwaka jana kwa maana itarahisisha kupunguza kwanza muda wa mgonjwa kwenda kwa daktari lakini pili elimu hii ama teknolojia hii itatibu wagonjwa wengi zaidi kwa sababu daktari anaweza akawa yuko Dar es Salaam anatibu wagonjwa ambao wako mikoani. Kama ambavyo mnafahamu madaktari tulionao ni wachache inabidi daktari mmoja huyohuyo awe fully utilized kutibu wagonjwa wengi zaidi kwa njia ya mtandao kwa maana kwamba mgonjwa anaenda sehemu ambapo kuna mawasiliano na anawasiliana na daktari wake through telemedicine. Kwa hiyo, ningefurahi zaidi kuona hii telemedicine inakuwa implemented hapa nchini Tanzania. Najua mmeshaanza pilot study lakini ni vizuri zaidi kuweza kufanya haraka zaidi kwa mikoa mingine kwa sababu wagonjwa wengi wanarundikana mahospitalini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine nikija katika suala la nishati kwa maana ya umeme, ukisoma katika Mpango wetu tumetilia mkazo zaidi kwenye umeme wa maji. Umeme huu wa maji kama mnavyofahamu kwamba unatokana zaidi na maji lakini wakati mwingine mazingira yanakuwa si rafiki sana kwa kuwa vyanzo vya maji huwa vinakauka kufuatana na mabadiliko ya tabia ya nchi ya dunia.

Kwa hiyo, ningependekeza kwamba ni vizuri sasa pia tukajikita katika umeme unaotokana na joto ardhi (geothermal), sijaona katika Mpango wetu hapa. Geothermal ni muhimu kwa sababu ule ni umeme ambao tunaita ni renewable tofauti na maji yakishatumika wakati mwingine kama vyanzo vimekauka na huku umeme hatutaweza kupata.

Umeme upo wa aina nyingi kuna ule wa upepo, wa gesi ambao tuko nao lakini nao bado haujawa effectively fully utilized pia ni vizuri tukaendelea kuu-utilize, kuna umeme wa solar energy, biomass energy lakini nikazie zaidi katika geothermal kwa sababu kuna maeneo mengi katika nchi yetu ya Tanzania geothermal ama jotoardhi umeme huu unapatikana. Zaidi katika umeme kuna hili jambo la bomba la gesi ningefurahi ama Watanzania wengi wangefurahi kuona bomba hili linaanza sasa kusambazwa mikoani kote na lisiishie tu Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nikija katika suala la maji, maji ni uzima, maji ni uhai, maji ni utu na maji ni roho. Waheshimiwa Wabunge wengi mmelalamikia hapa mara nyingi ukisoma ule ukurasa wa 32 tunaona kuna baadhi ya miradi ambayo itaendelea katika mpango ujao, ni vizuri katika Mpango wetu kama tutaunda chombo maalum kama ambavyo imeundwa TARURA kwamba chenyewe kijikite zaidi katika kuleta maji kwa maana ya vijijini na mijini. Sasa hivi kwa tafiti niliyoifanya nimeona Halmashauri nyingi sana hazina wataalamu na ndiyo maana miradi mingine mingi inashindwa kuendelea kwa sababu hamna ile M&E (Monitory and Evolution) katika ufuatiliaji wa miradi. Kwa hiyo, ombi langu ni kwamba kiundwe hicho chombo maalum kwa ajili ya suala hili la maji vijijini na mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikija katika suala la kilimo, ukisoma ule ukurasa wa 28 utaona kwamba kilimo kimetiliwa mkazo lakini wewe Mheshimiwa Waziri unafahamu kwamba sasa tuna shida kubwa sana na masoko ya mazao ambayo tumezalisha, kila zao bei yake imeshuka. Kwa mfano, ukichukulia mahindi yameshuka, viazi nichukulie mfano kwa mfano kule tulikokuwa tunalima nyumbani debe moja lilikuwa linauzwa shilingi 10,000 hadi shilingi 15,000 lakini sasa hivi debe moja ni shilingi 2,000 kwa maana ya gunia zima ni shilingi 10,000 badala ya shilingi 65,000.

Kwa hiyo, kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara katika Mpango wetu kama wataanzisha section ambayo itakuwa inatoa taarifa kupitia njia ya teknolojia kama simu whatever kwa wakulima wote, tuwe na database ya wakulima ambao wanalima mahindi, choroko na kila aina ya zao wanapewa taarifa kupitia hizo simu walizonazo ama hiyo database ili wawataarifu sehemu gani masoko hayo kwa sasa bei ipo juu. Kwa hiyo, kama Mpango huu ungezingatia hilo ingekuwa ni jambo zuri na lenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika kuwekeza kwenye kilimo tumeona mazao kama chai, mahindi na baadhi ya maeneo bei ya chai ipo chini sana, lakini wenzetu jirani Kenya iko bei za juu, kwa sababu wametafuta masoko nje ya nchiyao hasa hasa Uingereza. Kwa hiyo na sisi kama tungeweza kutafuta hayo masoko ingekuwa rahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikija katika suala la teknolojia, tumeona katika ukurasa ule wa kwanza wa mwongozo wa maandalizi wa mpango wa bajeti umezungumzia mifumo mingi ambayo itatengenezwa, mimi nitoe angalizo hapa. Tumeona teknolojia hii imekuja kwa kasi katika nchi yetu ya Tanzania pia nitoe angalizo kwa maana ya mifumo hiihiii ndiyo inatumika katika masuala ya udukuzi.

Kwa hiyo, lazima tuwe very sensitive sana tunapo- implement mifumo hii kwa kuwa hata wale wanaofanya programming, coding na vitu vingine vyote wanajua namna gani ya kuiba kupitia mifumo hii kwa kuwa mimi na wewe ambao ni end user hatuwezi kujua lakini kwa kuwa mimi nimeyaishi haya nafahamu. Kwa hiyo, ni vizuri sana haya mambo yazingatiwe katika Mpango wetu. Tusilete tu mifumo kama kuleta lakini tujue pia na consequences baada ya kutumia mifumo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeona katika hii mifumo kwa mfano hii ya EFD, EFD ni mifumo ambayo inatumika kukadiria mapato lakini risiti zake zile baada ya muda, ukinunua leo bidhaa ukapewa risiti baada ya wiki moja ama wiki mbili au mwezi zinafutika maana yake unakuwa hakuna tena ushahidi wa kusema wewe ulitumia ile EFD. Kwa hiyo, ni vizuri zaidi kama hizo integrated systems zitakuwa na mifumo ambayo inatoa risiti ambayo ni permanent. Kwa nini mfano ukitoa photocopy karatasi idumu zaidi wakati EFD ambayo ni ya fedha isidumu, kwa hiyo, nafikiri hilo pia mliweke vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwa kuwa hizi teknolojia ni nyingi wakati mwingine wanatumia commercial software ambazo ni gharama zaidi, tunaweza tukafikiri tunapunguza gharama lakini kumbe tunaongeza gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningeshauri watumie open software ambazo zinatumika nchi nyingi za Scandinavia na ambazo ndizo ziko applicable duniani kwa sasa, kwa sababu hizi commercial software ni gharama na tunakuwa hatujapunguza chochote kile zaidi ya kuongeza gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho katika suala la TEHAMA, ingependeza na ingefaa zaidi kuundwe Bodi ya wana-TEHAMA kama ambavyo kuna Bodi za Uhasibu, Bodi za Ukandarasi, kwa sababu teknolojia ndani ya nchi yetu inakuja kwa speed zaidi. Kama tutakuwa na hawa watu kwa pamoja maana yake itaturahisishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zingine kama Finland wameendelea zaidi kwa sababu waligundua ile Kampuni ya Nokia, ukienda Korea Kusini kuna Samsung, ukienda Marekani hivyo hivyo lakini tukiwa na Bodi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nami fursa niweze kuchangia katika hotuba hii ya Wizara TAMISEMI. Kabla ya yote, kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema ambaye ametupa nafasi na tumeweza kuamka salama na kufika ndani ya Ukumbi huu wa Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anazozifanya katika nchi hii ya Tanzania; na amekuwa role model pia wa Marais wengine wa Afrika na nchi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pasipo kusahau, niendelee kuwashukuru Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kwa namna wanavyofanya kazi vizuri. Kipekee sana, nakushukuru sana kaka yangu, Mheshimiwa Jafo, Waziri mwenye dhamana ya TAMISEMI kwa kazi nzuri na kubwa unayoifanya, nawe ukiwa kijana, umekuwa role model pia kwa vijana wenzako. Tunakushukuru sana na pongezi, tumeona namna ambavyo



unapambana kila kona. Vilevile kwa kusaidiwa na wasaidizi wako; Naibu Mawaziri Mheshimiwa Kandege pamoja na Mheshimiwa Kakunda pasipo kuwasahau Watendaji wote wa Wizara hii TAMISEMI, kwa maana ya Katibu Mkuu - Engineer Iyombe, Naibu Katibu Mkuu - Dkt. Zainab pamoja na wengine wote na Wakurugenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijikite zaidi katika suala zima la TARURA. Kwanza naipongeza Serikali kwa kuanzisha chombo hiki cha TARURA. Kimekuwa msaada mkubwa sana kwetu Wabunge tunaotoka majimbo ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema kwamba TARURA pamoja na kwamba imeanzishwa, lakini bajeti yake ni ndogo kwa maana ya kwamba ina urefu mpana zaidi na uchumi mwingi unatoka vijijini na malighafi nyingi zinatoka kule, lakini bajeti yake ni ndogo. Asilimia 30 kwa 70 kwa maana ya TANROADS, hii hakika hawataweza kufanya kazi yao na kufikia lengo tulilokusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali yangu sikivu kwamba kama itaridhia kupitia Waziri Mpango baada ya kuleta bajeti yake ya Wizara ya Fedha, ingekuwa asilimia 50 kwa 50 tuna uhakika kwamba chombo hiki cha TARURA kitaweza kufanya kazi zake sawa sawa na vile ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, kuna changamoto mbalimbali katika Jimbo langu la Busokelo. TARURA hii baada ya kuanzishwa mwaka 2017 tuna mahusiano mazuri sana na wale managers pamoja na coordinators wa Mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mahusiano hayo, barabara ambazo ziko ndani ya Jimbo langu kwa mfumo ambao sasa hivi tuko nao ni kilometa 475 kupitia District Roads Management Systems (DROMAS) ambako ndiko zinakuwa updated barabara zote 475. Bajeti ambayo



Halmashauri yangu inapata ni shilingi milioni 600.6. Sasa unaweza ukapiga mahesabu hapo kwamba kilometa 475 kwa shilingi milion 606 siyo kitu. Kwa msingi huo, kwa bahati mbaya sana pia hizi fedha ambazo zilipangwa bajeti ya mwaka 2017/2018 hazijakwenda kama ilivyokusudiwa, kwa maana ya kwamba imekatwa nusu kwamba alipe madeni ya zamani kwa maana ya kwamba ile mipango ambayo tulikuwa tumepanga kwa barabara zote hadi hivi ninavyosema, haijaweza kutekelezeka kwa sababu fedha hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naliomba pia Bunge lako Tukufu kwamba kwa umoja wetu hii TARURA lazima ipewe fedha nyingi za kutosha. Zaidi pia katika hizi barabara, kuna barabara ambazo hadi sasa hivi ninavyozungumza, wananchi wangu wamenipigia simu tangu juzi, wengine jana kwamba kuna kata ambazo hakuna mawasiliano kabisa. Kuna Kata za Mpata, Isange, Kandete, Rufilyo na maeneo mengine mbalimbali ndani ya jimbo langu, hakuna mawasiliano kabisa kwa maana ya hizi mvua zinazonyesha sasa hivi kipindi hiki cha msimu wa mvua, kumekuwa na changamoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yetu kwa sababu ni sikivu, wale managers wanapokuwa wanaomba fedha za dharura wapelekewe kwa haraka zaidi kwa sababu kunakuwa hakuna mawasiliano kabisa ya wale wananchi, maana wanaishi kama kisiwa. Wakiwa kama kisiwani maana yake hawawezi kufanya chochote. Ikumbukwe kwamba Mkoa wa Mbeya ni miongoni mwa mikoa ile tunayoiita big four ambayo inazalisha sana raw materials pamoja na chakula katika nchi hii. Kwa hiyo, kama hakutakuwa na uwezekano wa kusafirisha mazao yanayozalishwa kule kuja mijini, maana yake hata huku mijini pia tutapata taabu kupata hayo mahitaji tunayohitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika jambo hilo hilo la TARURA, naiomba Serikali, kwa kuwa Mkoa wa Mbeya, hasa Wilaya za Rungwe, Chunya pamoja na Busokelo, zinapata mvua karibu mwaka mzima, zaidi ya milimita 2,000 kwa



mwaka, tungetamani sana kama suala la kutangaza zabuni kwa wakandarasi zingeanza mwezi wa saba na wa nane ili wa tisa mkandarasi aanze kufanya kazi na wa kumi awe kazini, wa kumi na moja amalizie kazi. Ingetusaidia zaidi, kuliko sasa hivi wakandarasi wengi wamekimbia site kwa sababu mvua zinanyesha usiku na mchana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia ni suala la afya. Afya ni uzima na roho. Kwa kweli kipekee sana Mheshimiwa Jaffo nikupongeze tena sana, niipongeze sana Serikali yangu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi ambavyo mmejenga vituo vingi vya afya katika nchi hii ya Tanzania. Historia itandikwa kwamba kipindi fulani ndipo tulijenga vituo vingi vya afya. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, nipongeze pia suala zima katika Halmashauri yangu ya Busokelo, nimeona mmetutengea bajeti ya shilingi 1,500,000,000 kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Wilaya. Ninawashukuru sana katika jambo hili. Pia ikumbukwe kwamba katika maombi ambayo tuliomba, kuna kituo kimoja najua Mheshimiwa Jafo atakifanyia kazi, kinaitwa Isangi. Tulishaandikiwa barua na Mheshimiwa Waziri wa Afya, lakini hadi leo hii fedha hazijaingia. Ninaamini utalifuatilia na tutaweza kupata fedha hizi ili tuweze kuendelea kufanyia kazi hicho kituo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala zima la jengo la Halmashauri. Tunashukuru Halmashauri yetu mmeipa shilingi 2,300,000,000 kwa ajili ya kukamilisha jengo. Tunawashukuru sana katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nizungumzie kuhusiana na suala zima la utumishi. Watumishi wetu katika Halmashauri ya Busokelo limekuwa na shida na changamoto kubwa. Tuna upungufu wa watu takribani 516 katika Halmashauri yetu, kwa maana Halmashauri ni changa na watumishi 516 ni wengi kwa maana hawapo kazini. Wengine ndio hao wamefukuzwa na wengine hawana vyeti. Kwa hiyo,



tunaiomba Serikali kwamba maombi maalum ambayo Mheshimiwa tulikupelekea uweze kuyafanyia kazi na bahati nzuri mzee wangu nilikupelekea uweze kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, hatuna. Ofisi hii ilijengwa tangu mwaka 1930. Kwa maana hiyo, nazishukuru sana Kamati zote za Bunge ambazo zimepita pale, ninyi ni mashahidi. Kuna Kamati ya PAC, lakini pia Kamati ya Maendeleo na Huduma za Jamii, mmeona jengo lile kwamba limekuwa la miaka mingi. Tuiombe Serikali, tunajua kwenye mwaka huu hamjatenga fedha, lakini tukuombe Mheshimiwa Waziri kwamba mwakani tuweze kujenga Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ikizingatiwa kwamba Mbeya ni miongoni mwa mikoa ambayo pato lake la Taifa sasa hivi ni Mkoa wa pili baada ya Dar es Salaam. Kwa hiyo, ni vizuri tungeweza kuuboresha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuzungumzia ni suala zima la mifumo ya computer. Mimi nikiwa mdau, nimeona katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumzia mifumo mingi ya computer na wana mifumo mingi kweli kweli. Niwapongeze sana kwamba sasa nchi yetu inaenda katika digitali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningeweza kutoa mapendekezo ama maono kwa maana ya moja, mifumo hii mingi baadhi yake inatoka nchi za nje.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Nishati jioni hii ya leo. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametukusanyisha tena mahali hapa jioni hii tukichangia Wizara hii muhimu kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kipekee pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa namna ya kipekee kwa kazi nzuri anayowafanyia Watanzania, lakini pia kwa mikataba ambayo tayari tumeshaingia na wenzetu wa Uganda katika bomba hili la mafuta kutoka Uganda mpaka Mkoa wa Tanga. Kipekee pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya nishati pamoja na Naibu wake na Katibu Mkuu wa Wizara hii, wamefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba, Mheshimiwa Waziri wewe tangu umekuwa Naibu Waziri umeitendea haki Wizara hii, kipekee nitambue mchango wako mkubwa, natambua uipokuwa Naibu Waziri Wizara hii ilikuwa ina mapato ya bilioni 9 kwa wiki, leo hii Wizara inakuwa na kati ya bilioni 42 mpaka bilioni 47 ni hatua kubwa sana, lakini pia shirika lilikuwa katika hali ambayo si sawa kifedha, lakini hivi leo shirika linajiendesha lenyewe na baadhi ya miradi linaweza kusimamia lenyewe kwa fedha za ndani ni hatua kubwa sana hii Mheshimiwa Waziri, lakini jambo lingine pia nikupongeze pamoja na watendaji wako kwa kuchukua hatua; hivi karibuni umechukua hatua za kinidhamu kwa watumishi wote ambao hawafuati maelekezo ya Wizara. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine nataka nikupongeze kwa kusimamia vizuri miradi yote ya kimkakati ukiwemo mradi mkubwa wa Mwalimu Nyerere ambao utazalisha Megawatt zaidi ya 2,115 pamoja na miradi mingine mbalimbali ambayo Wizara inaanza kusimamia na kwa hakika mnastahiki pongezi nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nijikite zaidi katika umeme huu wa REA. Umeme wa REA umekuwa mkombozi mkubwa sana katika maeneo yetu katika nchi yetu ya Tanzania. Lazima tukiri Serikali imefanya kazi kubwa na kwa msingi huo Jimbo langu la Busokelo lina vijiji 56 na katika vijiji vyote 56 vimepata umeme vijiji 55, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. Na kwa msingi huo bado Kijiji kimoja tu cha Kilugu ambacho kipo Kata ya Itete, nikuombe katika awamu hii na mzunguko unaofuata nacho kipate umeme katika awamu hii inayofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, licha ya kwamba, vijiji 55 vyote vimepata umeme, lakini kuna changamoto katika kupeleka kwenye vitongoji. Katika kata ambayo ina vijiji vitano na katika kijiji kimojawapo inaweza ikawa na vitongoji sita na katika vitongoji sita vinaweza vikapata vitongoji viwili; tunahesabu kweli kwamba, kijiji kimepata umeme, lakini vitongoji vinne vyote vinakuwa havina umeme. Naamini katika mipango ijayo basi tuwekeze zaidi katika vitongoji, ili vitongoji vyote sasa vya Tanzania tuone kwamba, tuna umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kila mmoja anafahamu kwamba, umeme ndio uchumi, umeme ni viwanda. Umeme ni nuru, umeme ni kila kitu katika maisha ya Mtanzania. Kwa maana hiyo, niipongeze pia Wizara kwa kuendelea katika kuratibu na kuzalisha umeme kwa kutumia njia jadidifu, hususan, renewable energies. Na nimeshuhudia miradi hii, geothermal, ikiwemo ambayo inaendelea kuchorongwa kule kwangu Jimbo la Busokelo tumechoronga vishimo vitatu na dalili zote za kuonesha kwamba, geothermal ipo kwa hiyo, lazima niipongeze sana Serikali kupitia Kampuni tanzu ya TANESCO, Tanzania Geothermal Development Company, ambayo inafanya kazi hiyo ya uchorongaji ni hatua kubwa sana hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo yote nataka pia nizungumzie Shirika letu la Petrol Nchini, TPDC. Tumeona gesi inavyozalishwa, lakini pili tumeona kutoridhishwa katika usambazaji wa gesi.

Mheshimiwa Spika, Bunge lililopita nilikuwa Mjumbe wa Kamati ya PIC. Tulitembelea maeneo mengi ambapo TPDC imepeleka gesi, tunawapongeza sana, lakini kasi yake ya kupeleka kwa wananchi bado hairidhishi. Kupitia hotuba hii Mheshimiwa Waziri, naomba sasa watu wa TPDC wajipange namna ya kupeleka cubic nyingi zaidi kwa wananchi. Kwa sasa hivi wamepeleka zaidi ya 733,521 futi za ujazo wakati wananchi zaidi ya milioni 50 tupo Watanzania kwa hiyo, waongeze kasi zaidi katika kupeleka umeme maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri utakapokuja tunataka ueleze kinagaubaga Wizara imetoa miongozo kwamba, umeme ni kweli 27,000/= lakini kuna baadhi ya maeneo umeme hawatozwi 27,000/=. Hii imekuwa ni changamoto na Wizara kadiri mnavyotoa maelekezo mara nyingi watendaji wenu wa chini hawawaelewi. Nafikiri kuna namna ambavyo mnaweza mkafanya ili waweze kuelewa kwa sababu, kama Serikali inapeleka umeme kwa 27,000/= lakini watendaji hawafuati hayo basi kutakuwa kuna namna ambavyo inatatakiwa mchukue hatua zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nataka nizungumzie ni suala la EWURA. EWURA mwaka 2018 niliweza kuchangia namna ambavyo wanaweza kusambaza ama wakatoa miongozo na kanuni, niwapongeze kwamba, sasa hivi wametoa miongozo na kanuni namna ambavyo hata vituo au magari ya kuuzia petroli ama dizeli yanaweza kufanya kazi, lakini baadhi ya maeneo ambamo hakuna petroli ama dizeli imekuwa ni changamoto kubwa sana na ukiwafuatilia watu wa EWURA wanakwambia kanuni zimekamilika, lakini utekelezaji ndio umekuwa ni changamoto.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba suala hili waharrakishe watu wa EWURA. Maeneo yote ambayo hayana mafuta, hususan peripherals, sehemu ambazo hakuna petrol stations, basi watumie njia mbadala ya magari maalum ambayo yana mita na yanaweza yakafanya biashara hii na Serikali ikakusanya kodi yake na pia tukapunguza gharama za wale watumiaji ambao wanatumia mafuta ya kwenye vidumu na wanaua magari yetu, hususan pump huwa mara nyingi sana zinakufa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nataka nizungumzie suala la umeme kukatikakatika sana. Katika Jimbo langu la Busokelo kwa siku unaweza ukakatika umeme zaidi ya mara 24 na sababu kubwa sana ya kukatika umeme kule ni kwa sababu upepo, mvua pamoja na miti mingi sana, lakini mwaka 2018/19 Serikali ilichukua hatua za kuweza kufyeka miti yote kwenye line. Hadi magimbi ya chini walifyeka, lakini tatizo hili mpaka leo bado lipo.

Mheshimiwa Spika, sasa ushauri wangu kwa Serikali, ikiwapendeza kwa sababu, maeneo yale ni mvua nyingi sana kwa mwaka mzima. Basi mjitahidi mje na solution ya kuwa na nguzo za zege, lakini pia ikiwezekana nyaya badala ya kupita angani zichimbieni chini ardhini kama wanavyofanya wenzetu wa nchi nyingine zilizoendelea; lakini zaidi Waziri mkija na wazo la kuwa na nguzo za chuma katika maeneo yote ambayo kuna changamoto ya kukatika-katika umeme kwa sababu za kijiografia ya hali ya hewa, basi hii itasaidia na kupunguza hii hali kwa sababu, umeme unapokatika Busokelo, Tukuyu, Rungwe, Ileje, Kyela, lazima hiyo line iwe affected kwa kukatika kwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine ambalo nataka nizungumzie ni suala hili la back-ups ama systems ama mifumo ya teknolojia kwa TANESCO. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, ulichukua hatua kubwa mara baada ya mifumo kusimama ama ku-stop kwa sababu tu back-ups hazikuwepo.

Kwa hiyo, nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na kama mdau wa ICT inasikitisha sana kuona kwamba, systems zinakuwa developed, lakini wanakuwa hawana back-ups. Na back-ups hizi kuanzia sasa, kitaalamu ama kitaaluma, inatakiwa isiwe katika jingo hilohilo la mifumo ilipo inawezekana wakaziweka hata Mwanza, hata Mbeya, lakini zikafanya synchronization ili ikitokea pengine any catastrophe ama janga lolote basi zile back-ups ziweze ku-take off halafu mifumo iendelee kufanya kazi kuliko kama ilivyotokea hivi karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho nataka nizungumzie jambo moja, ni muumini wa energy mix na Serikali yetu inafanya kazi hii ya energy mix. Ninachotaka kusema kwamba, tunaweza tukafikiri zaidi ya hapa, kuna mifumo mingi ya umeme duniani kwa hivi sasa; ukienda Japan kuna mfumo unaitwa co-diffusion new hydrogen energy, mfumo huu ni off grid. Inawezekana kwetu sasa tunaweza tukaanza kuufikiria hata kama hatujaanza kuutekeleza, lakini ni mfumo wa kutoa umeme kwa bei nafuu sana pasipo kutumia gharama ya kusafirisha nyaya kama tunavyofanya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naamini kupitia Wizara yako Mheshimiwa Waziri unaweza ukafanya tafiti kupitia wataalamu wako kwamba, umeme utoakanao na hydrogen energy ukoje kwa maana ya off grid kwa sababu, una faida nyingi. Kwanza hakuna nyaya kama tunavyofanya sasa, kwa mfano kama hivi Dodoma tungekuwa na umeme wa kwetu, Iringa wa kwao, hivyohivyo kwa hiyo, ingepunguza hizi distances za kusafirisha umeme umbali mrefu, lakini kukatikakatika, lakini zaidi mfumo huu unarahisisha kupunguza mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mwisho kabisa nishukuru sana Serikali kwa kutuletea umeme wa Lumakali ambao utazalisha Megawatt 222 katika Mkoa wa Njombe, Jimbo la Makete pamoja na Busokelo. Nina hakika utakuwa na fursa nzuri kwa Watanzania kwa ajili ya kuwekeza, lakini pia kwa ajili ya kuongeza katika uzalishaji wa umeme na viwandani hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa fursa, nikutakie kila la heri Mheshimiwa Waziri katika kutekeleza bajeti hii na mimi naiunga mkono asilimia 100 ili mkafanye zaidi ya hapa mlipofanya. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, nami ninakushukuru sana kwa kunipa wasaa huu katika kuchangia hoja iliyo mbele yetu, kwanza nianze kuunga mkono hoja hii.

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mungu wa Mbingu na Dunia aliyetufanya leo tujadili hoja hii muhimu ndani ya Bunge lako Tukufu. Shukrani zangu za kipekee ziende kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye ameendelea kuniamini kuwa Msaidizi wake katika nafasi hii ya Naibu Waziri sekta ya Uchukuzi kwa kipindi kingine tena. Shukrani zingine ziende kwa Mheshimiwa Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, zaidi Waziri wetu Profesa Mbarawa ambaye amekuwa Mwalimu mwema, ametufundisha na anatusimamia vema sisi Wasaidizi wake katika nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, zaidi pia Waheshimiwa Wabunge niwapongeze wote kwa namna ambavyo mmechangia hotuba hii ya bajeti ya Wizara yetu ya Ujenzi na Uchukuzi pamoja na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu pamoja na wote ambao wengine wamechangia kwa njia ya maandishi lakini wengi mmeongea. Pia familia yangu mama, watoto pamoja na familia kwa ujumla na wananchi wangu wa Jimbo la Busokelo ambao wameniamini kwa kipindi hiki cha pili awamu ya pili kama Mbunge wao na Mwakilishi wa Jimbo la Busokelo.

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze katika hoja za Waheshimiwa Wabunge. Waheshimiwa Wabunge naungana nanyi kwa michango yenu yote ambao wamechangia katika Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi. Nakumbuka Bunge kama hili la mwaka jana na mwaka huu ni tofauti sana, kwa kweli tunawashukuru sana na nitaanza kujielekeza katika ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR.

Mheshimiwa Spika, tunampongeza Mheshimiwa Rais tangu amepata nafasi ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu amesimamia vyema sana miradi yetu hii ya SGR. Wakati anaingia madarakani katika lot ya kwanza ilikuwa asilimia 83.55, hivi sasa ni asilimia zaidi ya 98.1. Lot Namba Mbili kwa maana ya kutoka Morogoro hadi Makutupora ilikuwa asilimia 57.57 sasa ni zaidi ya asilimia 93.4. Kwa kweli kazi imefanyika na kilometa zilizokuwepo zilikuwa ni 722 na sasa ni zaidi ya kilometa 1280 ambazo Mheshimiwa Rais katika awamu yake amesaini na thamani ya miradi yenye takribani zaidi ya trilioni 23.3 katika reli hii ya SGR. Kwa kweli tuna kila sababu ya kumshukuru na kumpongeza na vipande vinne vimesainiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutoa ufafanuzi kulikuwa kuna hoja za ni lini hasa SGR itaanza kufanyakazi. Reli hii ya kisasa kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro yenye kilometa 300, mara nyingi tumekuwa tukijibu swali hapa Bungeni, lakini nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba mabehewa yamekwishaingia baadhi lakini mengine mabehewa ya ghorofa kutoka Ujerumani yanaingia nchini ifikapo tarehe Mbili Juni na tunategemea kupata vichwa vya treni mwezi wa Julai. Kwa hiyo, mara tu baada ya vichwa vya treni kufika tunategemea huduma zitaanza kutolewa.

Mheshimiwa Spika, kipande hiki cha Dar es Salaam – Morogoro chenye kilometa 300 tunategemea kukamilika kwa kadri mkataba wetu ulivyo ni mwezi Septemba 2023. Kipande cha Morogoro - Makutupora tunategemea kukamilika Januari 2024 kwa sasa ni asilimia 93.83 ya mradi yenye kilometa 422.

Mheshimiwa Spika, kipande cha Makutupora - Tabora kinategemea kikamilike mwezi Desemba 2026 kwa sasa ina asilimia Saba yenye kilometa 368. Kipande cha Tabora- Isaka chenye kilometa 165 kwa sasa iko asilimia 2.39. kipande cha Isaka – Mwanza asilimia 31. 07 yenye kilometa 341. Kipande cha Tabora - Kigoma ambapo hivi sasa Mkandarasi yuko site na yupo kujenga camp.

Mheshimiwa Spika, kazi hii ya SGR imefanywa na wazawa wa kitanzania, Ma-Engineer wa Kitanzania ndiyo wame-design. Kupitia wataalam wetu na niwapongeze sana viongozi wote nikianza na Mkurugenzi Mtendaji wa TRC pamoja na Mainjinia wote walioshiriki katika design and building ya mradi huu ni mradi mkubwa kimkakati kwa hiyo tunategemea hata wenzetu wa ile reli ya kutoka Uvinza - Musongati mpaka Gitega yenye kilometa 317 hivi sasa mazungumzo yanaendelea Benki ya African Development imeonesha nia ya kufadhili mradi huu. Kwa hiyo, itakuwa kuna connection sasa kati ya reli na wa kwenda Kigoma pamoja na hii ambayo inaenda mpaka Burundi ambako kuna tani zaidi ya milioni 150 za nickel na ambazo tunategemea zisafirishwe kupitia SGR yetu. Takribani kwa mwaka tunakusudia, kwamba reli hii minimum itaweza kubeba tani milioni 17 kwa mwaka lakini maximum zaidi ya tani milioni 25. Kwa hiyo, niwapongeze wote wanaoshiriki katika ujenzi huu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ninalotaka nizungumzie zaidi ni suala hili la Reli ya Kusini. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia hapa Reli ya Kusini kwamba ni mkombozi na kweli nasi Wizara tumeliona hili. Reli ya Kusini kutoka Mbamba bay mpaka Mtwara. Tunatambua kwamba mizigo ama makaa ya mawe yanayosafirishwa na mizigo kutoka makaa ya mawe mpaka bandarini yanaharibu sana barabara zetu. Kwa maana hiyo Serikali imefanya nini?

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweza kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, hivi sasa tunatafuta fedha kwa njia ya ubia ili reli hii ianze pia kufanya kazi kama ambavyo reli ya kati tunayoijenga.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna hoja za ni lini hasa wakati mwingine behewa zile zilizokuja baadhi ya Wabunge walikuwa wanasema siyo yenyewe. Sasa nataka niwahakikishie kwamba kuna set za treni za kisasa EMU maana yake Electrical Multiple Unit kwa lugha nyingine tunasema treni zilizochongoka vichwa vyake navyo vitawasili hapa nchini ifikapo Machi, 2023.

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie Watanzania wenzangu kwamba reli hii inakwenda vizuri na tuko vizuri kwamba itakamilika kwa wakati kama ambavyo nimeeleza.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilikuwa ni reli ya TAZARA. TAZARA ni muunganiko kati ya Tanzania na Zambia. Tarehe 14 Machi Waheshimiwa Mawaziri wetu kupitia Baraza la Mawaziri walifanya kikao. Changamoto kubwa reli hii ilikuwa ni suala la sheria iliyopo na wenzetu waliomba tuwape nafasi kwa sababu ni Serikali mpya, kwa hiyo wana-review sheria zote za nchi yao ikiwemo na hii ya TAZARA. Hatukuishia hapo tu baada ya kuona wenzetu wana-review hiyo sheria na sisi tayari tulishaanza maandalizi na tulisha-review lakini hatuwezi kufanya maamuzi lazima tuwashirikishe kama ambavyo mkataba wetu ulivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nini ambacho kipo sasa hivi? Ni kwamba reli ya TAZARA tumeunda timu tatu, timu ya Mawaziri wa Tanzania na Zambia, timu ya Makatibu Wakuu pamoja na Watendaji Wakuu. Timu hizi kazi yao kubwa ni kuratibu zoezi hili la transition period kwa sababu tayari kuna wawekezaji ambao wameonesha nia kuishirikisha sekta binafsi ikiwemo wenzetu wa China kwamba wanaweza kuwekeza katika reli hii ya TAZARA.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ninalotaka nizungumzie zaidi ni suala zima la meli za Ziwa Tanganyika. Waheshimiwa Wabunge wa Mikoa yote hususan Mikoa ya Kigoma, Rukwa pamoja na Katavi na asubuhi hapa nimejibu swali kuhusiana na suala la Meli za Ziwa Tanganyika. Tumepokea ushauri wenu kwamba, badala ya kuwa na meli moja kubwa ambayo inabeba watu 600 na tani 400 tunategemea tufanye vile ambavyo mmeshauri. Ina-make sense kwamba tukiwa na meli mbili ambazo zinaweza zikawa zinapishana na kwa kuwa bado tuko katika kipindi cha majadiliano, ushauri wenu umepokelewa na Serikali tutaufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kuna meli zingine ambazo tunaendelea kuzikarabati, kwa mfano meli ya MV Liemba pamoja na MV Mwongozo. Mv Liemba tunasaini makataba mwezi ujao wa Sita na MV Mwongozo tayari Mkandarasi Mshauri ameshapatikana ambaye ni TMA, kwa hiyo nao wanaanza kazi rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo limezungumzwa sana hapa ni suala la viwanja vya ndege nchini. Baadhi ya Wabunge wamechangia suala la kwamba ndege zetu nchini ikifika saa kumi na mbili wakati huo huo zinakwenda kulala na binadamu tunakwenda kulala. Sasa nini kifanyike? Ni kuweka taa katika viwanja vyetu vyote nchini ili ndege zifanye kazi masaa 24.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia jambo hilo katika bajeti ijayo 2022/2023 viwanja vifuatavyo vinakwenda kufungiwa taa. Kiwanja cha Arusha, Iringa, Msalato, Kigoma, Sumbawanga, Shinyanga, Lake Manyara, Tanga, Lindi. Kwa sababu kwa sasa, viwanja ambavyo vina taa ni vichache sana, kiwanja cha JNIA, kiwanja cha KIA, kiwanja cha Zanzibar, Mwanza, Tabora, Songwe, Songea na Mtwara. Kwa hiyo, maombi yenu na namna ambavyo mmechangia bajeti hii mjue kwamba, katika mipango yetu na kwa kuwa baadhi ya viwanja tayari tumeshasaini ni miongoni mwa maeneo ambayo tunakwenda kuweka taa katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna changamoto ya kiwanja cha Bukoba. Kiwanja cha Bukoba tumekipangia fedha kwa ajili ya kujenga control tower kwa maana ya kuongozea ndege pamoja na mifumo ya kuongozea ndege inayoitwa Instrument Landing System na hii mifumo itafungwa maeneo yote.

Mheshimiwa Spika, tuwaombe Waheshimiwa Wabunge watupitishie bajeti yetu ili haya yote ambayo ninayasema hapa yaweze kutekelezeka. Kulikuwa pia kuna jambo la miradi ya kimkakati ambayo Mheshimiwa Waziri wangu atakwenda kuizungumzia. Kwa hiyo, katika haya kulikuwa kuna jambo pia la umiliki wa ndege ambayo pia Mheshimiwa Waziri wangu ataenda kuzungumzia hususan kati ya ATCL pamoja na TGFA.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikushukuru sana kwa muda huu, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa namna ya kipekee ambavyo wameweza kuchangia bajeti yetu na naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hotuba hii ya Bajeti ya Serikali Kuu. Niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi Rehema aliyetupatia uhai hata kuchangia kwenye bajeti hizi zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi yake nzuri iliyotukuka ya kuwatumikia Watanzania. Nina sababu nyingi sana za kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi hii ambayo anaifanya, maana amefanya, amefanya na ameendelea kufanya na kuzidi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja nyingi za Waheshimiwa Wabunge ambazo zimekuja katika Wizara yetu ya Ujenzi na Uchukuzi, Sekta ya Uchukuzi. Nitaanza kutoa ufafanuzi baadhi ya hoja nikianza na Taasisi yetu ya Usafiri wa Nchi Kavu (LATRA). Kulikuwa na hoja ambayo inasema mabasi ya abiria kusafiri masaa 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la saa 24, tumekaa na wenzetu wa Jeshi la Polisi na baada ya kujiridhisha kwamba usalama upo, tukatoa masaa kwamba yaanze kusafiri saa 11.00 alfajiri badala ya saa 12.00. Baadaye tukatoa tena, baadhi ya mabasi yapatayo 68 kwamba tuanze kusafiri kuanzia tisa alfajiri na hii inafanyika. Tunakoelekea ni baadhi ya mikoa. Tunategemea mikoa yote tuanze kufanya hivi, lakini hadi hapo tutakapopata taarifa kamili za kiusalama kwamba inaruhusiwa kusafiri masaa 24. Kwa hiyo, tumeanza kama pilot study lakini tunaendelea na hadi hapo tutakapoanza kusafiri kwa saa zote 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na hoja nyingine ya TRC kuhusu miundombinu ya Reli ya MGR. Ni kweli kwamba reli yetu ya kisasa inajengwa, na pia tuna reli ambayo ndiyo inafanya kazi hivi sasa. Tumeendelea kuiboresha na kuikarabati hususan katika maeneo ya kutoka Kaliua – Mpanda ambapo imegharimu takribani zaidi ya shilingi bilioni 357 na mkandarasi yupo site na njia ya kutoka Dar es Salaam mpaka Tabora tunaendelea kuikarabati. Kwa maana hiyo, hadi kutoka Tabora – Kigoma tutaendelea kuikarabati kwa kuwa pia kuna mkandarasi ambaye yuko site kwa reli hii ya MGR.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kulikuwa kuna hoja za SGR ya kutoka Dar es Salaam – Morogoro yenye kilometa 300. Tayari tumefanya kwa asilimia 98.14 na 2% zilizobaki ni kwa ajili ya kuunganisha pale bandarini. Tuna hakika ifikapo mwezi wa Tisa mwaka huu, kadiri mkataba ambao tumesainiana na mkandarasi, eneo la kutoka Stesheni Kuu - Posta kwenda Bandarini litakuwa imekamilika. Hivyo asilimia 100 ya reli hii kwa kipande hiki cha Dar es Salaam – Morogoro kilometa 300 kitakuwa kimekamilika chote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumepokea mabehewa ya kisasa ya mfano na ya ghorofa ambapo mabehewa haya yataanza kutumika ifikapo mwezi wa Saba mwishoni, mara tutakapokuwa tumepokea vichwa vya umeme vya kuendeshea mabehewa haya. Kwa hili nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu katika historia ya nchi ya Tanzania, tutaanza kutumia mabehewa ya ghorofa ya kisasa na bora kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoka Morogoro mpaka Makutupora yenye kilometa zaidi ya 422 tuko asilimia 93. Tunategemea pia ifikapo mwakani reli hii tutakuwa tumeikamilisha na kutoka Makutupora – Tabora kilometa 368 tupo 7%, kutoka Tabora – Isaka kilometa 165 tuna 3%, Isaka mpaka Mwanza kilometa 341 tuko asilimia 31 na kutoka Tabora mpaka Kigoma tayari mkandarasi yupo site na anaendelea na mobilization kwa maana ya kujenga camp. Hii yote ni kutaka kuunganisha pande zote za nchi yetu kutoka Ziwa Victoria mpaka Dar es Salaam baharini; kutoka Ziwa Tanganyika mpaka Dar es Salaam baharini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo hata kwa wenzetu wa Mtwara Corridor (ushoroba wa Mtwara) mara nyingi imeulizwa maswali hapa kwamba ni lini reli ya SGR itaanza? Nataka niwahakikishie mikoa yote ya Mtwara, Lindi pamoja na Ruvuma kwamba reli hii yenye kilometa 1,000 ilishafanyiwa upembuzi yakinifu. Sasa tayari makampuni zaidi ya kutoka nchi tano yameonesha nia ya kuwekeza katika reli hii. Kikwazo kikubwa ilikuwa ni kwa namna gani sheria yetu ile ya ubia tuweze kuiboresha. Tayari ile sheria imeboreshwa na Waheshimiwa Wabunge mliipitisha wiki iliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa kazi iliyopo, mara baada ya Mheshimiwa Rais kusaini sheria hii, tayari wakandarasi na makampuni kutoka hizo nchi wapo kutoka Uingereza, Marekani, Afrika Kusini, Croatia, Morocco na nchi nyingine. Wote wameonesha nia ya kuja kuwekeza katika Standard Gauge katika mikoa hii ya ushoroba wa Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la meli katika Ziwa Tanganyika. Waheshimiwa Wabunge wa Mikoa ya Kigoma, Rukwa na Katavi, ninyi ni mashahidi, tumekaa kikao takribani zaidi ya masaa matatu mpaka usiku kujadili ni namna gani wananchi wetu waliopata shida kwa miaka mingi na wengine wengi wamepata changamoto ya usafiri katika Ziwa Tanganyika, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Bajeti ya mwaka ujao imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa meli kubwa mbili za kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ushauri wa Waheshimiwa Wabunge katika maeneo hayo, walishauri badala ya kuwa na meli moja ya kubeba abiria 600 na tani 400 ya mizigo, ni bora tuwe na meli mbili. Hili ndilo ambalo limetufanya tusisaini mkataba ambao tayari tulishampata mkandarasi, lakini ile meli ya mizigo yenyewe tutaendelea kuitengeneza na pia tutaendelea kusaini mkataba wake. Kwa maana hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge katika mikoa hiyo kwamba katika Bajeti ijayo, nina hakika kwamba tunakwenda kuboresha usafiri katika Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na suala la viwanja vya ndege. Waheshimiwa Wabunge wengi wameuliza, kwa nini ndege zetu ikifika saa 12.00 jioni, muda wa giza ukiingia nazo zinatua? Katika Bajeti ijayo tunakwenda kukarabati viwanja visivyopungua 15 na vingine ambavyo vinafanya kazi sasa. Tunaanza na kiwanja cha kwetu hapa Dodoma ambacho hakina taa. Sasa hivi taa zilizopo ni za solar, haziwezi kufanya kazi masaa 24. Kwa hiyo, kuna mkandarasi ambaye sasa hivi anaweka taa za kuongozea ndege usiku na mchana. Ifikapo mwezi wa Nane kiwanja hiki kitakuwa na taa, na tuna hakika tutakuwa tunatua usiku na wakati wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikoa mingine ambayo tunakwenda kuboresha viwanja hivyo ni pamoja na Mkoa wa Lindi na Iringa ambapo yuko mkandarasi. Kwa awamu ya kwanza Serikali imetoa fedha, lakini awamu ya pili Benki ya Dunia ndiyo itakayokamilisha majengo pamoja na kujenga control tower. Vile vile kuna Mkoa wa Tanga, Sumbawanga, Kigoma, Musoma, Bukoba ambako tutajenga control tower, kuna Mkoa wa Arusha ambapo tunategemea tujenge taa za kuongozea ndege, nako hakuna taa, na pia kubadilisha runway kwa sababu iko karibu sana na barabara, ile barabara tutaihamishia upande wa pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna eneo la Chato, Msalato, Moshi ambako kuna mkandarasi lakini naye tutaendelea kumwezesha ili akamilishe Kiwanja cha Ndege cha Moshi Mjini. Kuna Shinyanga, Kahama, Mpanda, Songwe, Songea, Mtwara, JNIA, Mwanza na Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni tumepokea ndege ya mizigo yenye kubeba tani 54. Ni furaha iliyoje kwamba sasa ndege yetu itaanza kazi rasmi kuruka katika maeneo mbalimbali kwa maeneo ambayo tumekubaliana kuanzia tarehe 26 mwezi huu wa Sita. Tutaanza kuruka kwenda Kinshasa, Comoros, Lusaka, Harare, India, Dubai, Lubumbashi pamoja na Entebbe. Hii ni fursa kubwa kwetu kwa kuendelea kuwekeza katika mazao, kwa maana ya ndege hii itakapokuwa inabeba mizigo, tunategemea tukauze, lakini pia kuwe na mizigo ya kuja ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona tushiriki kuchangia katika hotuba hii katika haya ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wameuliza. Pia kuna reli ya kisasa kutoka Uvinza – Msongati – Itega yenye urefu wa kilometa 367 ambayo inafadhiliwa, ama itajengwa kwa ufadhili wa African Development Bank na tayari tupo katika hatua za manunuzi. Lengo kubwa la reli hii ni kwenda kuchukua malighafi zilizopo nchini Burundi (Nickel) na kuunganisha na reli yetu ya kisasa itakayokuwa inajengwa kutoka Tabora kuja Kigoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja na ahsanteni sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Serikali Mtandao wa Mwaka 2019
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenye Muswada huu wa e-Government pia niipongeze sana Serikali kwa kuja na wazo hili la Serikali Mtandao. Mimi ninaamini kwamba ni wakati sahihi na ni wakati muafaka kwa sababu kila jambo lina mwanzo halafu unaendelea na progress na ninaamini hivyo kwa sababu nimeyaishi maisha ya IT, ICT na nimeyafanyia kazi kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ningeanza kwa kuuchambua Muswada kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Muswada huu una umuhimu mkubwa. Umuhimu wake umadhihirika kama ambavyo Kamati pia ya Bunge imeeleza pia Sheria yenyewe ama Muswada wenyewe unajieleza vizuri, nami ningetamani niongezee mengine ambayo hayapo kwenye Muswada kwamba pengine ungeenda extra mile zaidi hasa katika suala zima la E-government pamoja na masuala mengine ya kimtandao.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba siku hizi dunia ni kama kijiji, dunia iko kiganjani na umuhimu wa Muswada huu unadhihirika pale ambapo biashara na viwanda kwa kutumia njia ya mtandao utafanyakazi lakini kuna huduma za kifedha, kuna huduma za umeme, kuna huduma za simu, kuna utafiti wa maendeleo ya kisayansi, kuna kilimo, kuna afya, kuna ardhi, kuna elimu, kuna maji, kote huko TEHAMA inaingia.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu zaidi kwa sabbau TEHAMA siku hizi wenzetu duniani kote wanatumia TEHAMA katika sekta mbalimbali na sekta hizo ambazo nimezitamka hapa nikianzia na suala la elimu naamini kwa sababu e- Government itakuwa inasimamia suala la E-Learning (distance learning). Leo hii tunaona Open University ni miongoni mwa Vyuo Vikuu ambavyo vinafanyakazi vizuri katika Nchi yetu ya Tanzania kuvishinda hata Vyuo vile ambavyo wanafunzi wanakwenda field na bado ninaamini kupitia Muswada huu kwamba kutakuwa na integration kati ya vyuo vya Tanzania na vyuo vya nje kupitia e-Government ili wafanye connection na coordination kwa taasisi lakini pia na course ambazo zitakuwa hazitolewi hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kupitia Muswada huu ninaamini, kupitia e-Government, biashara mtandao (e- Commerce) itafanyakazi vizuri na leo hii wakulima wetu wengi wanalima, wanazalisha lakini masoko yao yanakuwa hafifu ama hawapati taarifa zilizo sahihi. Naamini kupitia e- Government watapata taarifa zilizo sahihi na kwa wakati pia kujua masoko duniani yanakwendaje. Hii ni rahisi tu kwa sababu Serikali inakuwa na database ya wananchi wake wote na wote wanaotumia simu haijalishi iwe ya Android ama ni simu ya kawaida wanaweza wakapata taarifa kupitia sms bulk bundles na vitu kama hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia natambua kwamba matumizi ya TEHAMA kwenye sekta ya afya Serikali imeshaanza kufanya naipongeza na inaweza ikaenda extra mile zaidi kwenye masuala la telemedicine. Nimekuwa nikizungumza habari za namna gani Daktari mmoja anaweza akatibu wagonjwa zaidi na popote ndani ya nchi ya Tanzania na hili limefanyika na ninaamini wanaweza wakaenda zaidi kwasababu hii telemedicine ni pale Daktari kwa mfano anakuwa Dar es Salaam anaweza akahudumia moja kwa moja mgonjwa aliyeko Mwanza, ama Kigoma, ama Mbeya, ama Zanzibar kupitia e-Government.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii ninaamini kuna kitu sasa hivi kipya kinaitwa Extension for Health, Community Health Care kwa maana kwamba wale wataalam wa afya anaweza akawa Daktari yuko Dar es Salaam anashauriana na kesi mbalimbali katika vituo vya afya, ama hospitali za Wilaya, ama za Mkoa, ama Rufaa na wana-share na wakati mwingine kwa kuwa mfumo huu unaruhusu kupiga picha yule mgonjwa halafu yule Daktari akapata specification ama akapata description za huyo mgonjwa lakini zaidi watapata maarifa at the same time badala ya kusafiri umbali mrefu kumhudumia mgonjwa na wakati mwingine huwa wanapoteza maisha wakiwa safarini.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini kupitia e- Government, uchumi wa kidijitali (digital economy) utafanyakazi vizuri. Leo hii tunapoteza mamilioni ka mabilioni ya fedha kupitia matangazo ya mtandao ambapo Serikali haipati kodi yake. Kila mmoja anaweza akatangaza kwa njia ya website, anaweza akatangaza kwa njia ya simu, anaweza akasoma lakini wenzetu nchi zilizoendelea ukienda Marekani kuna Amazon, ukienda China, ukienda maeneo mengine mbalimbali duniani biashara ya uchumi wa kidijitali imeshamiri kila kona.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii unaweza ukawa ume-order bidhaa yako kutoka Marekani ama China na ikakufikia pale ulipo, kwa nini Tanzania tusipeleke bidhaa zetu, huduma zetu nje ya Tanzania kwa njia hii ya TEHAMA.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika Muswada limezungumzwa suala la kwamba kila ambapo kutakuwa na miundombinu ya kujenga majengo lazima pia wa- consider infrastructure ya TEHAMA. Naamini hili litakuwa na muhimu na la msingi sana kwa sababu leo hii majengo mengi yanajengwa yanakuwa hayapewi kipaumbele kuweka infrastructure ya TEHAMA. Ninaamini pia kama watafanya consideration pia ya ulinzi na usalama katika maeneo hayo, kwa maana ya kwamba camera na vitu vingine itarahisisha zaidi suala zima la TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ningetamani sana nizungumze masuala mazima ya security katika Muswada huu. Security ni muhimu sana katika Nchi yetu ya Tanzania. Tunakwenda katika digitali na humu wameandika kitaalam zaidi kuna vitu kama firewalls ambayo inakuwa ndani ya software kwa ajili ya kuzia wale wadukuzi wa taarifa muhimu na kupeleka sehemu nyingine na wakati mwingine wana-develop viruses ambazo zinakuja ku-explore ama kuja kupata taarifa kwenye simu yako ama computer yako na kupeleka sehemu nyingine. Mimi ningeshauri kwamba eneo hili likaziwe mkazo zaidi na tutumie wataalam wetu wa hapa nchini na ndiyo maana Muswada umekuja kwa wakati, naipongeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika softwares hizi tunazo- develop ningetamani sana tutumie kitu kinaitwa open source software. Open source software itaipunguzia Serikali gharama kubwa kuliko ilivyo sasa. Mara nyingi kuna software kama Microsoft Office tunanunua, tuna-import wakati tungeweza kutumia mbadala kama Openoffice ambazo ni free na license yake ni free mwaka mzima lakini Microsoft Office kila mwaka inabidi u-renew inategemeana na license key ulizonazo. Vilevile kuna software nyingi tu mbali na Microsoft Office, kuna software kama Ach ambazo zinatumika katika masuala mazima ya ardhi, management information systems, kuna software kama postgresgl upande wa backup ya database, kuna Linux, kuna Apache, kuna tomcat, kuna software nyingi sana ambazo tunaweza tukazitumia sasa badala ya kununua na maintenance yake inakuwa gharama zaidi tukinunua kwa sabbau lazima mtahitaji watu ambao wametengeneza hizo software na kila mara mtahitaji kununua licenses ambazo haitakuwa salama kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima lingine ambalo ningetamani kuzungumza ni suala zima la Strong Data Backups. Leo hii tuna Data Center ambayo iko pale Kijitonyama Dar es Salaam na ninaamini tukiwa na backups sehemu tofauto tofauti za nchi ambazo zinafanya synchronization kila iitwapo leo itakuwa ni jambo la muhimu zaidi kuliko kutegemea Data Center moja ambapo kunaweza kutokea catastrophy zozote zile labda matetemeko ya ardhi, ama kuungua kwa moto wa majengo tunaweza tukapoteza data nyingi sana ambazo tumetumia gharama kubwa kwa ajili ya kuzipata. Kwa hiyo, ningeshauri kwamba tuwe na data center maeneo tofauti tofauti ambazo zitakuwa zinafanya synchronization na kuwa kitu kimoja.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ningeshauri mifumo yote ya Serikali hasa mifumo ya malipo inayotumika ngazi ya TAMISEMI iwe na uwezekano wa kuwa katika offline mode, in case kama kuna changamoto ya internet basi mifumo ile isisimame kufanyakazi iendelee kufanyakazi, ikifika internet wakati wa usiku ama wa saa ngapi pengine saa nane, saa tisa iweze kutuma data zile ambazo ziko offline mode kwenda kwenye server ambazo zimeshakuwa stored somewhere, kuliko hivi leo kama hakuna mfumo basi hata malipo yoyote hayawezi kufanyika. Ninaamini ikichukuliwa ile inaweza ikawa jambo muhimu zaidi.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ni muhimu zaidi ni suala zima hili la Bodi ya Taaluma ya ICT. Pamoja na kwamba bodi ipo itakayosimamia e-Government lakini taaluma yetu ya watu wa ICT hatujulikani, kila mmoja yuko kivyake. Natamani Serikali ije na kuwa na bodi moja itakayowaunganisha wana taaluma wa ICT ili wote tuwe kama zilivyo taaluma zingine za Engineering, kuna watu wa Accounts, kuna Wanasheria na wengine, sasa hivi kwa kuwa ulimwengu na TEHAMA ndiyo kichocheo kikubwa kwenye sekta zote za maendeleo, hatuna sababu ya kutokuwa na Bodi ya ICT Tanzania kama zilivyo Duniani. Kwa mfano kuna Sisco Satisfied Network Associate, kuna Sisco Satisfied Network Professionals, kuna levels tofauti ndiyo maana tunaona Mataifa mengine yameendelea kwasbabu watu wa IT, ICT wametambuliwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ningetamani ku-share pamoja na Serikali ikachukua ushauri huu ni suala zima hili la sharing data online na approval. Tumezungumza hapa kwamba wakati mwingine makaratasi yanakuwa mengi, napongeza Bunge lako kwamba limeanza sasa litakuwa kidijitali na kwa mfumo huo ninaamini kwamba hata Serikali ifanye ku-approve documents zake kwa njia ya mtandao. Suala zina la ku-save time na ku-save cost ndipo itakapofanyakazi hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini muda wangu umekwisha itoshe tu kusema naunga mkono sana Muswada huu ni Muswada muhimu kwa Taifa letu kama ambavyo yalivyo Mataifa yaliyoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, Ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu katika uchumi wa nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uzima na afya njema hata tumepata kufika kuiona siku ya leo. Nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kumwongoza vema Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na leo hii anafanya kazi iliyotukuka katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimshukuru Mungu pia kwa jinsi Mawaziri wanavyofanya kazi vizuri, Mawaziri wote, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na Watendaji wengine. Lakini kipekee sana niwashukuru baadhi ya Mawaziri ambao walifika Jimboni kwangu, nikianzia na kaka Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, ulinyeshewa sana na mvua kipindi kile! Pia Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya, pamoja na Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo, tunawashukuru sana! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nichangie kama ifuatavyo:-
Nikianza na suala la uwanja wa ndege wa Songwe, uwanja huu umejengwa zaidi ya miaka 14 sasa, tangu ambapo ulipendekezwa, tunashukuru Serikali ilipofikia, lakini bado unahitaji kuboreshwa zaidi! Uwanja huu ni muhimu sana kwa sababu unaunganisha Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini iwe Mbeya, Njombe, Katavi, Rukwa na Ruvuma, tunautumia uwanja huu wa Songwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja huu wa Songwe, nilikuwa nasoma kwenye vitabu umetengewa shilingi bilioni 10, lakini bilioni 10 hii naamini kwa suala la kujenga taa pamoja na kujenga ujenzi kwa maana ya fence, hakika Mheshimiwa Waziri hazitatosha kwa bajeti ambayo imetengwa pale! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini uwanja huu utakapojengwa, utafungua fursa nyingi sana za kiuchumi Nyanda za Juu Kusini. Wawekezaji wengi sana ambao wamekuja ili wawekeze, lakini wanasema hatuwezi kusafirisha mizigo kutoka Mbeya, ama kutoka Songwe, ama kutoka Njombe mpaka kwenda Dar es Salaam halafu ndipo iende Ulaya, wanataka ndege Emirates zitoke huko ziende moja kwa moja Mkoani Mbeya kwa ajili ya kuchukua hizo raw products na pia ziweze kuwa processed. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia uwanja huu ni muhimu kwa sababu kuna baadhi ya viwanda ambavyo vilikwishaanzishwa pale, vinashindwa kuendelea kwa sababu hakuna njia madhubuti; ukiangalia TAZARA, nayo haifanyi vizuri. Kwa hiyo, tunaomba uwanja huu uweze kukamilika kwa wakati ili uweze kufungua fursa nyingi za kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikija katika suala la barabara, suala la barabara kwa Jimbo langu la Busokelo ni changamoto kubwa sana. Nakumbuka kuna barabara ambayo iliahidiwa ni zaidi ya miaka 12 sasa inasemwa itajengwa kwa kiwango cha lami. Nikichukua kitabu cha Ilani ya Chama chetu ukurasa wa 49, hii ni Ilani ya Chama mwaka 2015 imeandikwa ile barabara pale kwamba Katumba – Mbambo - Tukuyu, kilomita 80 kwa kiwango cha lami, lakini kwa miaka yote hiyo hata hivi ninavyoongea, nakumbuka nilishawahi kuleta swali na Mheshimiwa Naibu Waziri, alilijibu kwamba ifikapo mwaka huu mwezi Septemba ama Oktoba itakuwa imekamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, tukija katika bajeti ukifungua ule ukurasa wa 243, imeandikwa upgrading to DSD of Katumba-Lwangwa- Mbambo- Tukuyu road kilometa 83, lakini hapa inaonyesha ni kilometa moja tu! Tunamwomba sana, Mheshimiwa Waziri, barabara hii ni ya enzi na enzi, alikuja Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa aliahidi, lakini alikuja Mzee, Mheshimiwa Dkt. Kikwete aliahidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 28 Agosti, 2015 Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, saa sita na dakika thelathini mchana aliahidi barabara hii na wananchi walipiga sana makofi wakiamini kwamba itajengwa. Hakika tunawaombeni sana, kwa sababu barabara hii, kule tuna vitu vingi kwanza kuna gesi asilia. Hii gesi asilia, kuna viwanda viwili ambavyo vinafanya extraction na exploration za minerals, lakini zinaharibika kwa sababu barabara haziko imara!
Mheshimiwa Naibu Spika, si gesi asilia tu, kuna suala zima la geothermal, karibu tutaanza kuchimba, umeme wa kutumia joto ardhi pia unatoka kule! Nakumbuka alipokuja Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo yeye mwenyewe alijionea ile barabara hadi akauliza Mheshimiwa Mbunge hapa vipi, nikasema na mimi nitalia kilio kwa Mheshimiwa Waziri wa Miundombinu ili aweze kutuwezesha kwa barabara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hivyo tu, hivi ninavyoongea Mheshimiwa Waziri, barabara ile nilipita mwezi wa nne hakika ilikuwa ni worse, worse, worse, nusura nipate ajali! Watano walikufa kwa sababu ya mvua ambazo zimenyesha sana kipindi hiki. Kwa hiyo, tunaomba mtukumbuke, mtukumbuke kwa maana ya kwamba, sehemu ambapo ilitakiwa tusafiri umbali wa kilometa pengine 20 inatulazimu tuzunguke sana. Kama mnakumbuka kipindi ambacho kumetokea mafuriko ya kule Kyela, watu wa Kyela wanalazimika kupita Ipinda, waje Mbambo, waje Masoko, waje Tukuyu wanatumia barabara hii na ndiyo kiunganishi pekee cha Halmashauri zote tatu, maana yake Halmashauri ya Rungwe, Wilaya ya Rungwe, Busokelo na Kyela. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaombeni sana na si hivyo tu, ni zaidi ya tani 20 kama si 30 zimeharibika wiki mbili zimepita kwa sababu ya barabara kutopitika, kwa maana ya kwamba malori yameweza kuzuia njia na hakuna abiria anayeweza kupita pale na utelezi ni mkali sana. Kwa hiyo, wananchi ambao wanalima wanashindwa kwenda kupeleka mazao yao kwenda mjini kwa sababu hakuna magari yanayokwenda kule kuchukua bidhaa zao, kwa hiyo tunawaombeni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini siyo hivyo tu, kuna suala zima la madaraja. Madaraja ni changamoto kubwa, ni changamoto kubwa kwa sababu sasa mvua zilivyonyesha zimesababisha baadhi ya madaraja hayo kuondoka, kwa maana ya kwamba wananchi wanatumia tunaita madaraja utepe. Sasa baadhi ya wanafunzi hawawezi kwenda ng‟ambo ya pili ya mto kwenda kusoma kwa sababu hawawezi kuning‟inia kwenye zile nyaya ama zile kamba ambazo zimewekwa pale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba kama kuna emergency plan yoyote iweze kutusaidia ili haya madaraja yaweze kujengwa hasahasa daraja la Nsanga. Halafu kuna daraja ambalo lipo Kata ya Kisiba ambalo linaitwa Kibundugulu, hii Kibundugulu imesababisha hata kwenye mitandao, ambao mna WhatsApp, baadhi ya akinamama wanatembea juu ya kamba, inasikitisha sana! Kwa mfano, kama huyo mama ni mjamzito kwa vyovyote vile hawezi kuvuka pale kwa sababu inahitaji apite mmoja baada ya mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaombeni sana Wizara hii kupitia Wizara ya Miundombinu mtusaidie kutengeneza hata emergency, wakati bado tunaendelea kusubiri hiyo long plan kwa ajili ya kutusaidia kujenga madaraja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na hayo, pia kuna suala hili la mitandao ya simu; mitandao ya simu ina-diverge sana kulipa kodi na kwa bahati mbaya sana pengine sijui tuna mtambo ama hatuna mtambo, lakini ni muhimu kupitia TCRA wawe na mtambo ambao unaweza uka-filter ama ukajua ni kiwango gani cha course ambazo kila siku zinaingia na kiwango gani cha mapato hata kama ni hizi M-pesa, Tigo pesa ili Serikali ipate mrabaha wake sawasawa, iwezekanavyo. Kwa maana hiyo basi, ni muhimu kuanzisha mitambo kama nchi zingine ambapo inarahisisha sana kutokuwa katika quarrels na Serikali kwa maana ya kufuatilia masuala ya kodi, mara hapa, mara pale, wewe unaingia tu kwenye system unajua bwana wewe umefanya hivi na hivi then lipa kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsanteni sana!
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kushauri Serikali kwenye Mpango wa mwaka 2017/2018 kama ifuatavyo:-
(i) Kilimo; kuongeza nguvu kubwa ya kuwasaidia wakulima kwa kuongeza pembejeo za kilimo na mbegu yenye ruzuku, kwa mikoa inayozalisha mazao mengi ya chakula na biashara.
(ii) Mifugo; ni muhimu kupunguza ama kuondoa kabisa migogoro ya wafugaji na wakulima, kwa kuwatengea maeneo maalum kwa ajili ya malisho ya mifugo yao.
(iii) Elimu; ni muhimu kwa Serikali kwa mwaka wa fedha 2017/2018 kuanza mean test mapema kwa ajili ya wanafunzi wa Vyuo Vikuu wanaoomba mikopo, ili kupunguza matatizo yanayotokana na kukopeshwa kwa wahitaji hao. Elimu ya shule zetu iwe ni kwa vitendo zaidi kuliko nadharia.
(iv) Afya; ni muhimu kupanga bajeti ya afya ambayo itakuwa inalenga kujitegemea kama nchi kuliko kutegemea wafadhili. Mfano, magonjwa kama ya UKIMWI, dawa zake zinategemea zaidi Global fund na President‟s Emergency Plan for Aids and relief from America (PEPFAR) ambapo Serikali bajeti yake ni kidogo sana na hivyo inaweza kupelekea maafa makubwa kama wafadhili hawa watajitoa na ukizingatia kuwa sera za nchi zao zinabadilika.
(v) Telemedicine; ni muhimu Wizara ya Afya kufanya matibabu kwa njia za mtandao yaani telemedicine.
(vi) Barabara (Miundombinu); kuna umuhimu mkubwa wa kujenga barabara ya kutoka Katumba-Lwangwa –Mbambo-Tukuyu iliyopo Mkoani Mbeya Wilayani Rungwe. Barabara hii inatakiwa kujengwa kwa kiwango cha lami ili wananchi wa Majimbo yote matatu yaani; Busokelo, Kyela na Rungwe wanufaike kwa kuweza kusafirisha mazao mbalimbali kama ndizi, mpunga, kokoa, viazi mviringo, chai, mbao, mahindi na mazao mengine mengi, lakini pia usafirishaji wa gesi asilia aina ya carbondioxide (Co2).
(vii) Geothermal (Nishati ya Umeme); ni muhimu kama nchi kuweza kuanza kuwekeza kwenye umeme wa joto-ardhi ambao unapatikana Jimbo la Busokelo, Wilaya ya Rungwe, Mkoa wa Mbeya eneo la Kata ya Ntaba.
Mheshimiwa Naibu Spika, nategemea mapendekezo yangu yatapewa kipaumbele.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa na mimi
niweze kuchangia katika hoja iliyo mbele yetu, ya Kamati ya Miundombinu. Kwanza niipongeze
kamati kwa jinsi ambavyo wameleta taarifa ambayo iko vizuri na ipo very detailed pamoja na
Mwenyekiti wa Kamati hii. Nina mambo machache ya kuweza kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ni suala la viwanja vya ndege, nikisoma ukurasa wa
17 inaonesha kabisa viwanja vya ndege vingi katika nchi yetu vinaendelea kujengwa. Lakini
kuna viwanja ambavyo vilikuwa vilikuwa vinaendela kwa muda mrefu hadi sasa hivi
wanapoleta hii ripoti havijapelekewa pesa hata senti.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na kiwanja cha ndege cha Songwe. Kiwanja cha
ndege cha Songwe mwaka 2015/2016, kilitengewa shilingi bilioni tano lakini hawakuletewa
fedha hizo, mwaka 2016/2017, tumetengewa bilioni saba hadi wanaandika ripoti hii
hawajaletewa hata senti tano, maana yake nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanja hiki, ni mfano mzuri kwa mikoa ya Nyanda za Juu
Kusini, Mkoa wa Mbeya, Rukwa, Katavi, Njombe, Iringa mpaka Songea. Kwa maana nyingine
kwa wale wote ambao wanatumia ndege zinazokwenda Mbeya ni hivi karibuni ni majuzi tu
fastjet imerudi kwa sababu ya kutoweza kutua katika kiwanja kile. Imerudi kwa sababu ukungu
ambao unatanda eneo lile, hakuna taa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nchi na kama Taifa tunataka tuwekeze zaidi katika
masuala ya viwanda, na wawekezaji wengi wanataka watumie usafiri huu wa njia ya ndege
kwa ajili ya kuja kuwekeza viwanda vyao hapa nchini. Kwa hiyo, naiomba Serikali kwamba, kwa
bajeti ambazo zimetengwa katika viwanja ndege mbalimbali kati nchi hii; ukizingatia
Mheshimiwa Rais, nampongeza kwa sababu ameshanunua ndege nyingi katika nchi hii, na
bado tunaendelea kununua kama Serikali. Kwa hiyo, viwanja hivi viweze kupelekewa fedha zao
kwa wakati na viweze kutengenezwa kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine muhimu zaidi ni suala la barabara kwa za
kuunganisha kwa kiwango cha lami. Nizipongeze Serikali ya Awamu ya Nne na ya Tano zote
zinaendelea kuthubutu kuunganisha maeneo mbalimbali katika nchi yetu kwa ajili ya
kuunganisha wananchi, lakini pia kwa ajili ya kuwawezesha wananchi kiuchumi. Nimuombe pia
Mheshimiwa Waziri, kwamba kuna barabara ambayo imeahidiwa mara nyingi, na nimeisema
hapa Bungeni kwa miaka mingi; barabara ya Katumba - Lwangwa - Mbwambwa - Tukuyu,
kilomita 83, na wewe Mheshimiwa Naibu Waziri uliona jinsi ambavyo wananchi tulipokea kwa
furaha na tupo tayari hata kutoa maeneo yetu kwa ajili barabara iweze kujengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la mawasiliano. Mawasiliano katika nchi
yetu yamekuwa kwa haraka sana, lakini jambo ambalo linasikitisha kidogo kwa wenzetu hawa
wa TCRA kumekuwa na utapeli mkubwa sana kupitia mawasiliano ya simu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba Wizara, lakini pia na wataalam,
kuna wataalam wazuri katika nchi hii ambao wanaweza wakaishauri Serikali ni mechanism gani
zitumike kwa ajili ya kuwabana wale wote ambao ni matapeli kwa njia ya mawasiliamo na
ninaamini kwa kuwa na mimi pia niko kwenye fani hiyo tunaweza tukasaidiana na watu wengi
kuiwezesha Serikali ili wananchi wake wasitapeliwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la umeme/nishati. Nakupongeza sana
Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo pamoja na Naibu wako kwa kazi nzuri mnazozifanya.
Suala la REA III na REA II imekuwa ni changamoto katika baadhi ya maeneo.
Mheshimiw Naibu Spika, mara nyingi Mheshimiwa Waziri umekuwa ukisistiza kwamba
wakandarasi wanapokuja katika maeneo yetu lazima wawasiliane na viongozi ambao ama ni
Waheshimiwa Wabunge ama Madiwani. Lakini kwa bahati mbaya sana wakandarasi
wanakwenda eneo…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nipo. Kwanza nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambazo anazifanya katika nchi yetu ya Tanzania. Tumeshuhudia jinsi ambavyo anajenga flyovers, tumeshuhudia jinsi ambavyo nchi yetu imeingia mikataba ya kujenga standard gauge katika reli ya kati, tumeshuhudia jinsi ambavyo majengo ya hosteli Dar es Salaam yamekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wizara hii kwa upande wetu wa Busokelo kuna barabara ambayo inaanzia Katumba – Luangwa - Mbambo mpaka Tukuyu, ina urefu wa kilometa 83. Hata kwa haya ambayo tumepata si haba, tunakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jinsi ambavyo umeshiriki kikamilifu pamoja na wataalam wako. Bado tunaomba kwa kuwa kilometa ambazo umetupa sasa hivi bado hazijatosheleza zile kilometa 83. Kwa hiyo, tunaomba ikiwezekana katika bajeti yako uweze kutuongezea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona pia jinsi ambavyo Wizara inavyofanya kazi vizuri hasa katika suala la mawasiliano. Nitoe ushauri wangu katika mambo machache hasa TCRA. Tumeaona jinsi watu wengi sana tunatumia mifumo hii ya simu lakini kwa bahati mbaya inatumika hata kwa njia ya uhalifu na TCRA wanashindwa kudhibiti na hata wakati mwingine watu wanatuma meseji za kutukana wenzao, kwa hiyo tulitaka mifumo hii iboreshwe vizuri ili wawe na mfumo ambao unaweza uka-filter, maana kila utakapokwenda TCRA wanakwambia hatujui ama mfuate mwenye namba fulani. Kama kutakuwa na systems ambazo zinaweza zikafanya kazi vizuri, bila shaka uhalifu ambao unaendelea sasa hivi nchini kwa kutumia njia ya mtandao hautakuwepo tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichangie katika suala la mifumo ya kompyuta, ukisoma kitabu cha Waziri ukurasa wa 202, wamesema watajenga National Internet Data Center. Napenda nishauri kama Mtaalam wa Mifumo ya Kompyuta, unapojenga Data Center ya nchi ambapo mtakuwa mna-share information mbalimbali, haitakiwi iwe centralized sehemu moja, iwe decentralizide ili ikitokea in case kuna any emergencies zile backups ziweze kufanya kazi vizuri, kama nchi za wenzetu za Ulaya wanavyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri katika jambo hili la mawasiliano, mara nyingi sana katika nchi yetu tunatumia soft ambazo tunasema ni commercial, commercial kwa maana ya kununua hizo software, lakini kama tungekuwa tunatumia software ambazo ni open source na gharama yake ni ndogo ni rahisi kuzi –maintain kwa maana ya sustainability yake inakuwa ni kubwa kuliko hizi commercial software ambazo tunanunua kwa gharama kubwa na kuzi-maintain kwake ni gharama kubwa vilevile. (Makofi)

Kwa hiyo, ningeshauri Serikali ianze sasa kama Mataifa mengine ambayo yameanza hasa nchi za Ulaya Magharibi zinafanya hivyo, lakini ukienda Marekani wanatumia zaidi hizi microsoft ambazo ni gharama kuzi-maintain lakini pia kuna software nyingi ambazo ningeweza pengine kuzitaja kuna hizi Postgrace, Oracle, Square Server, Survey, GSMO, kwa sababu nimeishi nazo naweza nikaishauri Serikali iweze kufanya hivyo. Pia kuna software nyingi, kuna nyingine ambazo zinatumika kwa ajili ya kuisaidia nchi iweze kupata mapato yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe ni shahidi sasa hivi Serikali ikitaka kupata mapato mazuri kutoka kwenye mitandao ya simu lazima waende kwenye mobile operator mwenyewe kwamba sasa mwezi huu umepata kiwango gani, wakati ilitakiwa wawe na mfumo ambao wao wanapeleka direct. Kwa hiyo, kila muamala unaofanyika either uwe wa pesa ama uwe wa simu Serikali iwe inajua kwa kiwango gani inaweza kupata mapato yake kupitia kwenye mifumo hii ya simu. Kwa sasa hivi Serikali inaibiwa sana kwa sababu hatuna hiyo mifumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi za wenzetu ambazo zimeendelea sasa ukienda kama Ethiopia, Afrika Kusini na nchi nyingine za Ulaya wana mifumo ambayo inakuwa centralized siyo kama sasa hivi ambavyo imekuwa decentralized. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niweze kumalizia kwa upande wa TBA. TBA inafanya kazi nzuri na nimeambiwa pia kwamba mmepewa kazi ya kujenga majengo ya Halmashauri mbalimbali nchini. Kwa bahati mbaya sana TBA katika baadhi mikoa hampo ikiwemo hata kule kwetu katika Jimbo la Busokelo, katika mkoa mzima wapo watatu tu. Kwa hiyo, fedha za Halmashauri nyingi mpya ambazo zimepewa zipo tu kwenye akaunti za Halmashauri na karibu mwaka wa fedha unakwisha. Tunapofuatilia na kufuatilia wanakwambia wamepewa kazi TBA. Kwa hiyo, tunaomba kama TBA watajenga na kwa kweli wanajenga kwa kiwango kizuri na kwa gharama nafuu, basi iongezewe uwezo zaidi ili iende hadi huko mikoani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, napenda kuunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia kwenye Wizara hii kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Busokelo lipo Mkoa wa Mbeya, Wilaya ya Rungwe. Kwa bahati mbaya sana miundombinu ya barabara haipo vizuri. Jimbo hilo tunalima mazao mbalimbali, kwa mfano, ndizi, kokoa, chai, viazi mviringo na vitamu, mihogo, mahindi, ufugaji wa ng’ombe wa maziwa, kilimo cha matunda, maparachichi, upasuaji wa mbao na shughuli zingine mbalimbali. Hata hivyo, miundombinu ya barabara ni mibovu sana, imesababisha mazao mengi kuoza, kuharibikia shambani na hivyo kuwafanya wananchi wa Busokelo kuwa maskini kwa sababu ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara tunazoomba kupandishwa hadhi ziwe chini ya TANROAD Mkoa wa Mbeya ni zifuatazo:-
(i) Barabara ya Lwangwa – Tiete-Lufilyo (kilomita15).
(ii) Barabara ya Kanyelele (Gesi) – Mpata –Ipembe –Suma (kilomita15).
(iii) Barabara ya Kyejo (Gesi) – Lwangwa (kilomita 5.7).
(iv) Barabara ya Lugombo-Bujingijira – Ngumbulu - Mbeya Vijijini (kilomita10).
(v) Barabara ya Itete – Kisegese – Ntaba - Ngeleka - Matema (kilomita 30).
(vi) Barabara ya Kilasi – Kitulo (Livingstone) - Makete (Njombe) (kilomita 30).

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya lami kutoka Katumba (Tukuyu) - Lwangwa - Mbambo Tukuyu, tunaomba sana iendelee kujengwa kwa kiwango cha lami kutoka Busokelo – Isange - Katumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu TCRA waweke mifumo ya kukusanya kodi toka kwa mobile operators. Mheshimiwa Mwenyekiti, Uwanja wa Ndege wa Songwe. Uwanja huu ni muhimu sana kwa Nyanda za Juu Kusini. Uwanja unahudumia Mbeya, Njombe, Rukwa, Katavi na Ruvuma pamoja na nchi jirani kama Malawi, Zambia, Congo na nyinginezo. Tunaomba kuwekewa taa za kuongozea ndege, kwa hali ilivyo hivi sasa, ndege haziwezi kutua wakati wa usiku na wakati wa ukungu na hivyo kusababisha hatari kwa abiria na usalama kwa ndege zenyewe. Aidha, naomba jengo la utawala lililopo Songwe limaliziwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuundwa kwa Bodi ya Wanasayansi waliomaliza masomo ya computer Science and Information Technology. Nchi yetu inapita kwenye sayansi na teknolojia. Asilimia kubwa ya pato la Taifa ni kutokana na mifumo ya IT. Napendekeza kuwepo na Bodi ya wana-IT ambayo itasimamia uvumbuzi wa teknolojia ndani ya nchi yetu kuliko kutumia wataalam kutoka mataifa ya nje kama ilivyo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, softwares & database; nashauri Serikali yetu ianze kutumia Open Source na STO Commercial Softwares ili kupunguza gharama za manunuzi na za uendeshaji. Kwa mfano, Postgress, SQL server, Geo- Network, Geo-Server, Survey Gizmo na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TTCL, National Internet Data Centre. Pamoja na kujenga data centre naomba iwe very strong na ijengwe maeneo tofauti tofauti ili back-ups ziwe mbali na systems.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali iliyo chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Busokelo ni jimbo changa na miundombinu ya maji ni tatizo kubwa sana, hasa Mji wa Lwangwa, Kandate, Ntaba na maeneo mengine. Miradi wa Masoko na Mwakaleli I na II ni miradi ya miaka mingi sana lakini hadi sasa haijakamilika. Kwa sababu hiyo, naomba Serikali iweze kutimiza ahadi ya viongozi wetu wa Serikali. Naomba majibu ya Serikali, ni lini Miradi ya Masoko, Mwakaleli I na II itakamilika?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa dhamira yake ya dhati kuhakikisha Serikali yake inamtua ndoo kichwani mama wa Kitanzania mijini na vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza pia Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu wake, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Wakurugenzi na watendaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia kwenye Wizara hii ya Maji kama ifuatavyo; maji ni uhai, maji ni roho, maji ni utu, yaana zaidi ya 65% ya mwili wa binadamu na maisha ya wanyama, mimea na binadamu yanategemea maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndani ya Jimbo langu la Busokelo kuna miradi ya maji ambayo inaitwa Mwakaleli I tangu mwaka 2009 hadi leo hii mradi huu bado haujakamilika na mkandarasi anasuasua kiasi kwamba hadi sasa chanzo cha maji hakijajengwa na wananchi wangu wanapata shida kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa kwenye Wizara hii ni ukosefu wa wataalam ngazi za Halmashauri na Mikoani inayosababisha miradi mingi kushindwa kuendelea na kusimama. Wataalam wa Halmashauri wapo chini ya Wizara ya TAMISEMI, lakini Wizara ya Maji ambao ndiyo wasimamiaji wakuu wa maji, hawana mamlaka juu ya wataalam hao Halmashauri na hivyo kupelekea kuwa vigumu kuwawajibisha wanapokuwa wamekosea. Ushauri wangu wataalam hawa wawe chini ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ya kuanzishwa kwa Wakala wa Maji Vijijini ili waweze kusimamia kwa ukaribu na ufasaha kuliko hivi ilivyo kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la miradi ya umwagiliaji limekuwa ni tatizo kubwa sana kwa wananchi wa Jimbo la Busokelo. Kuna skimu za umwagiliaji kwenye Mto Mbaka, Kata ya Kambasegela imesahaulika na kuna kituo cha umwagiliaji ambacho kilijengwa tangu mwaka 2009 hadi sasa hakuna mwendelezo wa aina yoyote na hivyo kuisababishia hasara Serikali maana kuna majengo ambayo tayari yalijengwa kama nyumba ya mtumishi, madarasa, mabweni ila bado bwalo tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ya kuongeza shilingi 50 kwa lita moja ya mafuta aina ya dizeli ama petroli.

Mheshimiwa Naibu Spika, wataalam wetu ngazi za Halmashauri ni muhimu wapewe/kuwezeshwa namna ya ku- design na ku-survey miradi ili zoezi hili lisitegemee wataalam toka Wizarani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Afya.

Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu tupo hapa kwa sababu ya afya na pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi ambavyo ameitendea haki Wizara hii ya Afya. Tumeona na tumeshuhudia ajira zikitolewa, tumeona jinsi ambavyo magodoro pamoja na vitanda vikipelekwa kwenye Halmashauri zote nchini, pia tumeona jinsi ujenzi wa chuo pamoja na hospitali ya Mloganzila kule Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zote hizi tunasema ahsante sana Mheshimiwa Rais pamoja na wasaidizi wake wakuu ambaye ni Mheshimiwa Waziri wa Afya Ummy Mwalimu pamoja na Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija katika Jimbo langu la Busokelo kuna changamoto ambazo mara nyingi nimekuwa nikiongea nawe Mheshimiwa Waziri kwa bahati mbaya sana hazijaweza kutekelezeka. Tuliomba mashine ya usingizi na kwa bahati mbaya pia tuna kituo kimoja tu katika Jimbo zima la Busokelo na mashine hii haipo, maana yake inawalazimu wananchi wangu kusafiri umbali wa zaidi ya kilometa 60 kufuata huduma mjini. Kwa hiyo, nitashukuru sana kama ambavyo uliniahidi kwamba unaweza kufuatilia na kutupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaomba sana katika hospitali hii ya Kandete tunasema kuna changamoto ya ultra sound na x-ray machine hatuna. Kwa hiyo, tunaomba kama mtaweza kutusaidia katika jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana kwa jinsi ambavyo mmejitahidi kupeleka dawa, lakini hizi dawa kwa bahati mbaya wakati mwingine ama yanachelewa kununuliwa katika Halmashauri zetu ama kunakuwa kuna technical delay hapo katikati. Kwa hiyo, tunaomba Wizara kama mtafuatilia vizuri na hii inakuwa ni nchi nzima. Wizara inatoa fedha lakini Halmashauri haziwajibiki ipasavyo. Kwa hiyo, katika hili nafikiri ingekuwa jambo jema kama tungefuatilia pia kama Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niwashukuru kwa ajili ya Hospitali ya Rufaa ya Mbeya. Hospitali ya Rufaa ya Mbeya tumeona jinsi ambavyo mmeipa kipaumbele kwa maana ya majengo pamoja na vitanda. Bado haitoshi hospitali hii kuna specialist ambao wapo pale kwa zaidi ya miaka mine, categorization zao za mishahara bado ni zilezile za zamani. Kwa hiyo, tungeomba hata hospitali nyingine katika nchi hii ambapo wamepandishwa ngazi kwa kusoma ama kwa taaluma yao waweze kulipwa kufuatana na jinsi ambavyo wanafanya kazi pale kazini kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie suala hili la TEHAMA kwenye afya. TEHAMA kwenye afya ni muhimu sana katika ulimwengu wa sasa, ukizingatia kwamba kwa sasa bajeti iliyopita Wizara mlipendekeza kwamba mtaanza kutumia tele-medicine. Tele-medicine ni mfumo ambao unatumika kutibu wagonjwa ama kufanya consultation na wagonjwa kwa daktari alie mbali na eneo husika. Anaweza akawa Dar es Salaam akamtibu ama akampa ushauri mtu ambaye yupo nje kabisa na Dar es Salaam labda mikoani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba hii tele- medicine iweze kuwezeshwa zaidi ili daktari aweze kupata nafasi ya kuhudumia wagonjwa wengi zaidi kuliko hivi sasa mpaka mgonjwa ama client aende hospitalini kutibiwa. Ni muhimu sana hili lizingatiwe kama Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningefurahi zaidi kuona database ambazo zinatumika hospitalini hasa hizi za CTC II ambayo ni Care and Treatment Clinic pamoja na DHIS II ambayo ni District Health Information Systems kama zinakuwa developed au programmed na wazawa kuliko hivi sasa wazawa wanashiriki kwa sehemu ndogo, asilimia kubwa sana tunapewa misaada kutoka nje kwa maana kwamba hata wale specialist wa kusimamia hizi. Lengo lake ni kufanya sustainability yake iweze kuwepo kwa sababu hii misaada kuna wakati itakwisha na ikiisha hatutakuwa tena na support nyingine yoyote. Kwa hiyo, tukiwashirikisha wazawa itaturahisishia zaidi kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nikija katika suala la HIV (UKIMWI) tumeona mmetenga shilingi bilioni 251.5; ninaiomba Wizara na Waheshimiwa Wabunge ninyi ni mashahidi, hivi karibuni tulikuwa na semina ya kutoka National Council of People Living With HIV humu ndani. Tuliona kwamba kuna changamoto kubwa sana kwa dawa kwa ajili ya magonjwa nyemelezi. Kwa bahati mbaya sana hizi opportunistic infections wafadhili hawatoi wala Serikali hainunui. Maana yake inaishia kuwa gharama kwa wagonjwa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja. Ahsante.
Azimio la Bunge Kuhusu Mapendekezo ya Kurejea Katiba ya Tume ya Usafiri wa Anga ya Afrika ya Mwaka 2009
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia kuhusu kuridhia Azimio hili la AFCAC. Naungana na Mheshimiwa Waziri pamoja na Kamati kwa namna ambavyo wameweza kuwasilisha jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili lina faida kubwa sana kwa nchi yetu, mpaka sasa tumechelewa. Kama ambavyo amesema Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake kwamba nchi zaidi ya 15 zimekwisharidhia, lakini sisi kama nchi bado hatujaridhia. Kuna faida kubwa sana kwa Taifa letu. Waheshimiwa Wabunge wengi hapa wameelezea faida ambazo zinatokana na kuridhiwa kwa itifaki hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge waweze kuridhia jambo hili. Faida zake zimeelezwa kinagaubaga ikiwemo suala la kukuza lugha yetu ya Kiswahili, katika Katiba limeelezewa vizuri kabisa. Ukiisoma Katiba yetu kuanzia Article 24 imeeleza lugha itakayotumika ni pamoja na Kiswahili. Kwa hiyo, tutakuwa na sifa muhimu kwa ajili ya kueneza lugha yetu ya Kiswahili kwa Bara zima la Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni pamoja na soko shindani. Mheshimiwa Stella Fiyao amesema hapa, kwamba tujipange kama Serikali. Nataka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kama Serikali tumejipanga vizuri kwa ajili ya kushindana na ndio maana na sisi kama nchi tunahitaji kuridhia ili tuendane na ulimwengu wa kileo. Kama tuliridhia mwaka 1969 na Katiba mpya ya 2009 tulisaini tangu mwaka 2010. Tulikuwa hatujaridhia kwa kipindi chote hicho tukisubiri wenzetu waweze kuridhia. Sasa nchi zaidi ya 15 zimeshasaini, maana yake sasa hivi sisi tuko nje ya mfumo ama hatuko ndani ya itifaki hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Watanzania wote kwamba kama Serikali tumejipanga vizuri katika soko hili shindani na hata ndege ambazo Mheshimiwa Rais amekuwa akitoa fedha kwa ajili ya kununua haziwezi kufanya kazi Tanzania peke yake. Tunahitaji kwenda kwenye mabara mengine, ili tukienda huko watalii waweze kuja lakini pia tufanye biashara na mataifa mengine. Hatuwezi kufanya hivyo kama jambo hili tutakuwa hatujaliridhia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho lakini sio kwa umuhimu, Mheshimiwa Dkt. Chamuriho pia alizungumza suala la ni namna gani tumejipanga kutokana na mkataba ambao ulisainiwa kule Senegal Yamoussoukro. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumejipanga kwa namna hii; kwanza, kuna mikataba kati ya nchi na nchi lakini pili kuna mikataba kati ya bara na bara. Kwa namna sisi tunavyofanya mpaka sasa tutatumia mkataba unaoitwa BASA yaani Bilateral Air Services Agreement. Hata sasa tunafanya hili, kwa hiyo tusiwe na mashaka kwamba pengine tukiridhia makampuni makubwa kama Emirates yanaweza kuja ndani ya nchi, halafu yakaanza kufanya shunting za ndege kwa mfano kutoka Dar es Salaam kwenda mikoani, hilo halitakuwa hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi Wizara hii ndiyo utii wa mgongo wa nchi yetu ya Tanzania lakini niwashukuru sana na kuwapongeza Mawaziri wote wawili mara nyingi sana nikiwa na changamoto huwa nawaona, Naibu Waziri amekuwa akinisaidia na Waziri amekuwa akinisaidia, kwa hiyo nawapongeza sana. Niwapongeze kipekee zaidi baada ya kutoa tozo katika mazao mbalimbali ambazo wakulima ilikuwa ni shida na changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri mchache kwa Serikali hasa tukianza na Jimbo langu la Busokelo ambako mara nyingi sana tunazalisha lita za maziwa zaidi ya 30,000,000 kwa mwaka lakini yanaharibika kabla hayajafika kiwandani kwa sababu hatuna kiwanda katika Halmashauri ya Busokelo. Tumejitahidi kujenga lakini tumeshindwa, tunaomba Serikali iweze kutusaidia katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hilo tu tunazalisha pia ama tunalima viazi mviringo, viazi vitamu, ndizi kwa wingi, mpunga na mazao mengine mbalimbali na hayo yote yanashindwa kufika sokoni kwa sababu ya miundombinu ambayo haiko rafiki kwetu. Kwa hiyo, tunaomba kama itawezekana kuanzishwa kwa viwanda vidogo vidogo katika maeneo yale kwa kuwa ninyi watu wa kilimo ndio wenyewe kwa sababu ninyi ndio mnaosimamia sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tozo ambazo zimetolewa hasa katika zao la chai. Zao la chai sisi ni wakulima wakubwa katika nchi hii ya Tanzania katika Wilaya ya Rungwe. Kuna hii tozo ambayo inaitwa gharama za uendeshaji wa vyama vya wakulima nafikiri kwa typing error imeandikwa ni Sh.5 lakini tozo hii ni Sh.9.50, ningeishauri Serikali isiiondoe kwa sababu kwanza hivi vyama ni vichanga na Serikali inahubiri habari ya ushirika. Sasa wakishawaondolea hawa maana yake watatawanyika kabisa hawatakuwa na nguvu yoyote ya kuweza kusimama na kulisimamia zao hili la chai, kuna kodi nyingi ambazo ningeshauri huko ndiko wangeweza kuondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda, zao la cocoa pia tunalima kule lakini hapa sijaona hata kidogo kutamkwa katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Naomba pia walizingatie kwa sababu ni muhimu na linaingiza fedha nyingi za kigeni kwa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pembejeo limekuwa likizungumzwa lakini nipongeze Serikali kwa sababu tumeamua kwamba ziletwe kwa bulk procurement. Wazo langu na ombi langu kwa Serikali kwamba katika nchi ya Tanzania kila sehemu tunazalisha ila kwa bahati mbaya majira yanatofautiana. Kwa hiyo, hata kama watanunua hizo pembejeo basi ziende kwa majira husika katika maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la TEHAMA na kilimo. TEHAMA na kilimo kwa nchi ambazo zimekomboka limekuwa ni msaada mkubwa sana katika nchi hizo. Hii TEHAMA itumike vizuri katika kuendeleza mazao mbalimbali nchini si kilimo tu hata uvuvi lakini pamoja na shughuli zingine zozote za kibinadamu zinazomwingizia kipato. TEHAMA inatumika namna gani? Kama sasa hivi tukijenga data center itapunguza gap kati ya watafiti wanaofanya tafiti pamoja na mkulima kwa sababu mtafiti mara nyingi anafanya tafiti lakini zile tafiti haziwasaidii wale wakulima wadogo wala wavuvi, wala wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kupitia TEHAMA maana yake watakuwa wanapata SMS direct kutoka data center hiyo kwenda kwa mkulima kama watakuwa na simu za mkononi tu inatosha kabisa. Kupitia TEHAMA pia tutapunguza majanga mbalimbali kwa kutoa taarifa kwa jamii mapema. Kwa mfano, mwaka jana tulikuwa na changamoto kubwa ya ukame, kama wakulima wa maeneo mengi wangepata taarifa kwamba kuna changamoto za ukame zinakuja kupitia simu za kiganjani mikononi mwao tusingekuwa na shida ya chakula katika maeneo tofauti tofauti katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu TEHAMA itasaidia zaidi kutafuta masoko. Kama Serikali itakuwa inasaidia kutafuta masoko dunia halafu wanatuma massage moja tu kwa wakulima fulani labda wa zao la pamba, chai, kahawa na mazao mengine maana yake itasaidia wale wapate taarifa mapema kuliko vile ambavyo kila mkulima mmoja mmoja anajitafutia soko lake pale anapoona yeye inafaa. Kwa hiyo, tukiwekeza katika TEHAMA najua na nina hakika kwamba wakulima wetu hawatakuwa kama walivyo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mchango wangu huu kidogo, naomba niunge mkono hoja, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Muswada wa Sheria ya Habari kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuundwa kwa ithibati ya wanahabari. Hii itasaidia kuwezesha tasnia hii ya habari kuheshimika kama ilivyo bodi za taaluma zingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuongeza hisa zaidi kwa wamiliki wa vyombo vya habari kwa Watanzania 51% na wageni toka nje 49%. Hii itasaidia sana uimarishwaji wa ulinzi kwa nchi na kupunguza habari zisizo za kweli kwa Mataifa ya nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bima ya afya. Muswada huu wa sheria unatoa umuhimu wa bima ya afya kwa wananchi wote na itawasaidia wakati wanapopata matatizo wakiwa kazini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri. Ningependa kushauri kuwa pamoja na umuhimu wa Muswada huu, ni vizuri tukazingatia umuhimu wa kuandika kanuni mapema ili baada ya Mheshimiwa Rais kusaini, sheria hii ianze mapema kutumika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono Muswada huu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Kabla ya yote kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anafanya maamuzi yaliyo mengi mazuri katika sekta hii ya uchukuzi na mawasiliano. Lakini pia niipongeze Wizara hii pamoja na Waziri, Naibu Mawaziri na watendaji wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa katika Jimbo la Busokelo ni barabara ambayo imeahidiwa kwa miaka mingi na Marais wote waliopita ukiachana na Baba wa Taifa ambayo ni Katumba – Lwangwa – Mbambo – Tukuyu yenye kilometa 85. Bahati nzuri sana nimeenda mara nyingi kwa Katibu Mkuu na amekuwa akiniahidi mara kwa mara lakini mara nyingi pia nimewasiliana na Waziri, nimepeleka mpaka maandiko lakini hadi hivi leo ninavyozungumza katika bajeti yake hakuna jambo ambalo limefanyika ambalo lilitakiwa lifanyike mwaka jana kwa bajeti ya mwaka 2017/2018. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni muhimu sana kwa wananchi wetu wa Busokelo na Rungwe kwa sababu kwanza gesi asilia aina ya carbon dioxide inapatikana kule lakini pia kuna aina mbalimbali ya mazao kama ndizi, viazi na maziwa kwa ajili ya ufugaji lakini barabara hii hata hivi ninavyozungumza wiki iliyopita tulikuwa na Mheshimiwa Waziri wa Nishati, tulikwama kwa zaidi ya dakika kadhaa kwa sababu ya barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Serikali na Wizara hii ichukulie umuhimu mkubwa barabara hii kwa sababu hata Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 28 Agosti, 2015 saa 6.30 pale viwanja vya Tukuyu Mjini aliahidi barabara hii kwamba ataitengeneza kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja kujibu useme kwamba barabara hii itaanza lini kutengenezwa kwa sababu mwaka huu wa fedha unakwisha na bajeti ilishatengwa hakuna lolote ambalo limefanyika, sielewi ni nini kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni barabara ya kutoka Luteba (Mbeya) – Makete – Njombe, ni barabara mpya ambayo inaunganisha mikoa yote miwili. Nikiwa Mbunge nimekuwa mbele pamoja na wananchi wangu kulima kwa jembe la mkono. Je, Serikali inatusaidiaje katika barabara hii kuhakikisha kwamba tunaunganisha mikoa yote miwili ya Njombe pamoja Mkoa wa Mbeya kupitia Luteba mpaka Makete. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali haitakuwa na fedha basi nikuombe Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wako na Katibu Mkuu twende wote tukalime kwa kushika jembe la mkono kwa sababu ninaona kila mara nikiandika hata maandiko tangu mwaka 2016 bado haya mambo hayaendi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, kuna barabara pia ya mchepuo wa kutoka Uyole kwenda Mbalizi barabara hii ni muhimu sana kwa wananchi wa Mbeya Jiji. Kwa sababu mahali pale katikati ya Jiji kumekuwa na foleni kubwa ukizingatia kwamba ule mji unakua kwa kasi. Kwa hiyo, tunaomba mchepuo wa barabara itakayoanzia Uyole kwenda Mbalizi na Songwe airport iweze kukamilika ili magari makubwa yawe yanapita ile diversion. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna jambo kubwa hili la Uwanja wa Ndege wa Songwe. Bahati nzuri sana Kamati yetu ya PIC tulikwenda kutembelea ule uwanja na kila mara nimemsikia Mheshimiwa Waziri hapa akijibu kwamba tunatengeneza taa za kuongozea ndege. Kwa bahati mbaya sana anasema ni shilingi bilioni nne lakini kwenye bajeti hapa ipo shilingi bilioni 3.7 na hizi fedha hazitatosha kutengeneza taa za kuongozea ndege pamoja na kujenga ukuta na runway, haitawezekana kwa fedha ambazo zipo hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuiombe Serikali kwamba iweze kutenga fedha za kutosha katika uwanja huu wa kimataifa na ikizingatiwa kuwa katika nchi yetu ya Tanzania kuna viwanja vikubwa vinne ambavyo vinaweza kusaidia viwanja vingine. Zaidi ya viwanja 54 vinahitaji kupata mapato kutoka viwanja vya Julius Kambarage Nyerere, Songwe, KIA na Mwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwahiyo, ningeishauri Serikali kwamba laiti kama tungeweza kuviwezesha hivi viwanja na vikaweza kukamilika ili fedha zile sasa ziweze kusaidia viwanja vingine ambavyo vipo kwenye mpango wa kutengenezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine muhimu ni suala la mawasiliano, katika sekta ya mawasiliano inachangia asilimia 13.1 ya pato la Taifa na kwa msingi huo tumeona mara nyingi database zetu ama software ambazo zinatumika katika mawasiliano zinatumia commercial software. Nikiwa mdau wa mawasiliano (TEHAMA) ningeshauri kwamba ianze kutumia open source kama vile Firefox, Fidora, Tomcat, http server na nyinginezo nyingi ili kuipunguzia gharama Serikali wakati wa kuendesha hii mifumo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu open source ni mifumo ambayo inakuwa ni wazi kwa maana kwamba own source code anaweza aka-edit mtu yeyote yule, lakini ukitumia commercial software maana yake unahitaji kununua license na zinakuwa na expiring date na running cost yake inakuwa ni kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niweze kuzungumzia suala zima katika suala hilo hilo la mawasiliano tumeona pia katika hii issue ya commercial software kuna baadhi ya pirates software ambazo zinatumika kwenye taasisi za Serikali ambazo hazijalipiwa license na gharama yake ni kubwa sana. Ni kubwa kwa maana kwamba wale ambao wanatengeneza software incase wakijua kwamba taasisi za Serikali zinatumia software ambazo hazina license, Serikali lazima itakuja kulipa fedha nyingi. Kwa hiyo, nitoe tahadhari hiyo kwamba haitakiwi tuingie kulipa huko wakati tungeweza kutumia hizi open source software.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninapenda kuunga mkono hoja, lakini nimuombe mheshimiwa Waziri aje na majibu yaliyo sahihi sana juu ya barabara ya kutoka Katumba – Luangwa – Mbambo – Tukuyu na ikibidi barabara ya kwenda Makete kutoka Busokelo twende wote tukalime kwa jembe la mkono kama fedha hazitapatikana hapa, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukizi na Mawasiliano. Kabla sijachangia, napenda kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ametupa uzima hata kuwepo siku hii ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano katika nchi nyingine na hata nchi yetu ya Tanzania ni muhimu sana kwa uchumi wetu wa Tanzania. Pia nianze kwa kumpongeza na kuwashukuru sana Mawaziri, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu pamoja na Manaibu Katibu Wakuu wote katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kwanza kwa kuzungumzia suala la barabara ambayo nimekuwa nikiizungumza humu Bungeni kwa muda mrefu, barabara ya Katumba – Lwangwa – Mbambo yenye urefu wa kilometa 83 na hii barabara ni mkombozi mkubwa sana kwa Jimbo langu la Busokelo pamoja na Majimbo jirani ikiwemo Kyela pamoja na Rungwe. Ni barabara pekee ambayo imeandikwa kwenye Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi kwa zaidi ya vitabu vitatu. Iliandikwa 2005, ikaandikwa 2010, iliandikwa 2015.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana kipekee Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivi karibuni tarehe 29 mwezi huu wa Tano alitembelea Halmashauri yetu ya Busokelo na kuahidi tena; na kuagiza Wizara kwamba sasa hii barabara itengenezwe kwa kiwango cha lami kwa kilomita zote 81.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Busokelo tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na wewe Mheshimiwa Naibu Spika ulikuwepo, ulishuhudia hali ya hewa ilivyokuwa, mvua zilikuwa ni nyingi na umuhimu wa barabara hii, kwa maana wananchi wote wanategemea barabara hii kwa sababu kule tuna viwanda vya chai, tuna viwanda mbalimbali ikiwemo gesi asilia (carbondioxide) lakini tunazalisha mazao ya kila aina, kwa sababu msimu wa mvua ni zaidi ya milimita 2000 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na barabara hiyo, kuna barabara nyingine ambayo inaunganisha Jimbo langu la Busokelo na Mkoa wa Njombe kupitia Makete na barabara hii nakumbuka mwaka 2018 Mheshimiwa Naibu Waziri, Eng. Kwandikwa alikuwa amekubali kwamba ataunga juhudi za wananchi wale kulima kwa jembe la mkono, lakini kwa bahati mbaya naona hakupata fursa hiyo. Naamini alikubali ili aiweke kwenye Bajeti ya Serikali ili sasa iweze nayo kuwa katika mpango mzima wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cha ajabu, bado sijaiona kwenye kitabu chetu hiki na ninaamini atakapokuja ku-wind up basi atakumbuka ile ahadi lakini na namna ambavyo wananchi wale walimwomba alivyokuja kutembelea ile barabara ya Mwakaleli mpaka kule Kandete. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na suala la barabara kuna jambo zima la miundombinu hasa upande wa uwanja wa Songwe wa Kimataifa. Uwanja huu shida kubwa na changamoto kubwa iliyopo pale ni suala la taa za kuongozea ndege. Nimeona kwenye kitabu hiki wameweka shilingi bilioni tatu kwa ajili ya kumalizia jengo la abiria pamoja na kuweka taa za kuongozea ndege wakati wa usiku na wakati wa mchana hasa wakati wa ukungu kipindi kama hiki, kwamba Mkoa wetu wa Mbeya mara nyingi unakuwa na shida ya ukungu muda mrefu. Kwa hiyo, ndege zinapata wakati mgumu kutua kipindi kama hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka mwaka 2018 pia mliweka kwenye bajeti haikutekelezeka, mwaka juzi iliwekwa haikutekelezeka. Naomba sana, hii shilingi bilioni 3.6 ambayo imewekwa sasa iweze kutekelezeka katika kipindi hiki. Nakumbuka mwaka huu alipokuja Mheshimiwa Rais kuzindua Kiwanda cha Maparachichi (Avocado Company) ambacho ni mkombozi mkubwa sana kwa wakulima wa Mkoa wa Mbeya pamoja na Wilaya ya Rungwe kwa ujumla, lakini maparachichi yale yanasafirishwa kwa njia ya malori mpaka Dar es Salaam ili yaweze kusafirishwa kwenda nje ya nchi. Siyo hivyo tu, yanasafirishwa mpaka Mombasa kwa sababu uwanja wetu wa Kimataifa wa Songwe hauna vigezo vya kufanya ndege za mizigo ziweze kutua pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kukamilika kwa kiwanja hiki cha Songwe kitafungua malango mengi sana ya fursa za kiuchumi kwa Mikoa ya Nyanda za juu Kusini lakini pamoja na Nchi za SADC kwa maana ya zilizo chini ya jangwa la Sahara na nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna suala zima la hizi hizi ndege ambazo sasa hivi tunapanda, wenzetu wanasema pengine hazina faida kwa sasa, lakini kawaida sekta moja inaweza ikawa na multiplier effect kwa sekta nyingine. Kwa hiyo, uchumi hauwezi kubadilika kwa sasa mara moja, pengine baada ya miaka mitano, 10, 20, 30 ndipo tutakapoona umuhimu wa hizi ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Wizara kwamba ikifungua malango kwa kufungua njia nyingine mpya za route kutoka hapa Dodoma kwenda Mbeya pamoja na Nyanda nyingine za juu Kusini ili mtu atoke Mbeya moja kwa moja kuja Dodoma na atoke Dodoma aende Dar es Salaam na maeneo mengine, lakini sasa hivi maana yake inakulazimu uende Dar es Salaam, uende Iringa then uende Mbeya ama utoke Dodoma uende Dar es Salaam then uende Mbeya moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka nizungumzie ni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru sana kunipa fursa nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Nishati. Awali ya yote kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutupa kibali kuwepo katika Bunge lako hili Tukufu. Lakini kipekee sana nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika Wizara hii ya Nishati na kwa Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wako mmekuja Jimboni kwangu Busokelo na mlifanya mikutano hata saa mbili usiku ilibidi kufanya ili tu wananchi wa Jimbo la Busokelo wapate umeme. Katika hili nawapongeza sana kwa niaba ya wananchi wangu Jimbo la Busokelo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina machache katika Wizara hii ya Nishati kwa sababu kwenye awamu ya kwanza REA III mzunguko wa kwanza Jimbo langu lilipata vijiji 50 kati ya vijiji 56 na katika hivi vijiji 50 ni vijiji 42 ambavyo vimepewa kipaumbele katika awamu hii ya REA III, kwa hiyo nipongeze sana Serikali katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba tumepata vijiji 42 kuna changamoto ambazo zimeambatana na mkandarasi kwanza kwa kuviacha vile vijiji 8 ambapo Mheshimiwa Waziri ulipokuja ulitoa amri na kauli kwamba lazima atekeleze vyote pasipo kujali aina ya nyumba ya nyasi ama si ya nyasi ama ya bati kwamba vyote vinastahili vipewe umeme.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ningependa kushauri katika jambo hili la kupeleka umeme katika huduma za jamii, kuna baadhi ya maeneo hasa hasa mashule, zahanati, hospitali, makanisa vimerukwa. Kwa hiyo, ningeomba katika awamu hii ambayo tunaingia mzunguko wa Awamu ya III wa REA viweze kupatiwa maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine mwenzangu ameshauri hapa kwamba kuna baadhi ya vitongoji hasa hasa umeme unapofika kwenye kijiji kimoja ambacho kina vitongoji vitano na kinafika kwenye kitongoji kimoja vitongoji vingine vyote vinne vinakuwa havijapata umeme hii inakuwa ni shida sana kwa wakazi jirani. Nafikiri katika mpango huu wa Awamu ya III mzunguko wa pili, ingefaa sana kwanza umeme unapofika kwenye kijiji basi na vitongoji vyake vyote viweze kupata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ningependa kushauri ni suala hili la miundombinu hasa hasa baadhi ya wakandarasi wanapopeleka hizi nguzo katika baadhi ya vitongoji ama vijiji, wanaweka karibu sana na miundombinu ya barabara na wakati mwingine watu wa TARURA wanapotaka kuanza kutengeneza zile barabara wanashindwa kwa sababu tayari nguzo zimeshasimama karibu kabisa na barabara nafikiri kungekuwa kuna umuhimu wa kushirikisha taasisi na Wizara zingine hasa hasa Wakala wa Barabara Vijijini ili wawe na umbali kiasi fulani ambapo itawezesha hizo nguzo ziweze kuwekwa badala ya kuweka karibu sana na barabara na baadaye inakuwa gharama tena ya kuanza kuzitoa maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ningependa kushauri suala la kukatika katika umeme Mkoa wa Mbeya na Wilaya zake zote ni miongoni mwa Mikoa ambayo umeme unakatika mara kwa mara na hasa katika Wilaya za Kyela, Rungwe, Busokelo, Mbeya Vijijini, Chunya, hadi Mbarali na hii yote ni kwa sababu ya miundombinu imechakaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba kwamba Mheshimiwa Waziri kwa sasa tuna teknolojia nyingi ya kusimika nguzo na kwa kuwa kule mvua nyingi zinanyesha karibia mwaka mzima na upepo unakuwa ni mwingi sana nafikiri tungetumia teknolojia ya kuweka nguzo ama nyaya kwa maana ya underground badala ya kuweka angani ambapo kila mara baada kupigwa na upepo ama ikipigwa na mvua ama na radi mvua umeme unakatika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine napenda kuzungumza suala la TPDC, TPDC ni shirika ambalo hakika mimi ni mjumbe wa Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma linafanya kazi nzuri na tumejionea sisi wajumbe namna ambavyo wameanza mchakato na kuona hata nyumba ambazo zinapata umeme kwa kupitia njia ya gesi. Pia tumeshuhudia hata magari ambayo yanatumia gesi ya Kitanzania, ambayo inachakatwa kule Mtwara. Kwa hiyo niwapongeza sana TPDC pamoja hata na wataalam ambao akinamama wapo pale ma-engineer na ni wazalendo Watanzania. Kwa hiyo niwapongeze sana uongozi wa TPDC pamoja na Kaimu Mtendaji Mkuu wa shirika hili.

Mheshimiwa Spika, changamoto ambayo wanayo TPDC hasa hasa katika suala zima la gesi asilia ambapo baadhi ya taasisi zingine zinapewa fedha kwa ajili ya kutengeneza miradi yao, lakini wao wanapewa fedha kwa maana ya kutengeneza mradi ambao fedha baadaye itakuwa claimed na TPDC.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mwakibete.

MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Kabla ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ametuwezesha kufika mahali hapa. Pili nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kwa kuniamini na zaidi pia niwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Busokelo kwa kunichagua kwa awamu nyingine tena ya pili, maana wanasema imani huzaa imani, nami nitawatumikia kwa moyo wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba zote mbili za Mheshimiwa Rais, ya kwanza nilishiriki 2015 na sasa ni 2020 na ndiyo maelekezo, ndiyo maagizo, ndiyo mtazamo wa nchi na hakuna ambaye anaweza kupinga hotuba hii kwamba ndiyo mwelekeo wetu wa nchi ya Tanzania kwa miaka mitano ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichangie hasa suala la ajira kwa vijana. Vijana wetu, wanafunzi wengi wanamaliza lakini ajira kwao ni changamoto. Ajira hizi zina uhusiano hasa hasa na sekta mbalimbali, si sekta tu ya kusoma, kama elimu ya Vyuo Vikuu, lakini na sekta zingine za kilimo, uvuvi, mifugo na sekta zingine mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na sekta ya uvuvi wa bahari Kuu; Bunge lako Tukufu mwaka 2018 lilitoa ripoti kuonyesha ni kwa namna gani ambavyo uvuvi wa Bahari Kuu hatuutumii vizuri, tunaita blue zone. Kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Rais ukisoma ukurasa 17, ameandika hivi: “Nchi yetu pia imebarikiwa kuwa na maeneo mengi yanayofaa kwa shughuli za uvuvi ikiwemo ukanda wa pwani, maziwa, mito na mabwawa. Hali hii inafanya sekta hii kuwa na nafasi ya kutoa mchango mkubwa kwenye kukuza pato la Taifa na pia kupambana na umaskini na tatizo la ajira. Hata hivyo kwa sasa mchango wake bado ni mdogo”.

Mheshimiwa Naibu Spika, tafsiri yake ni nini? Bunge lako mwaka 2018 liliunda tume ambayo ilishughulikia masuala ya uvuvi wa Bahari Kuu na ikatoa ripoti kwamba hivi sana kwa miaka tisa Serikali imekusanya takriban bilioni 29.7, kwa wastani wa mwaka maana yake ni sawasawa na bilioni 3.3. Hotuba ile pamoja na ripoti ile imeonyesha Tanzania tukitumia vizuri kina kirefu cha bahari tuliyonayo, tuna uwezo wa kukusanya mapato kwa mwaka takriban bilioni 353. Hapa mimi nakuja na taarifa muhimu na natamani Waziri wa Mifugo pamoja na Uvuvi azisikilize takwimu hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kina cha Bahari ya Hindi kama tutakitumia vizuri kwanza kuna samaki wanaoitwa tuna ama jodari kwa wale ambao wanatoka maeneo hayo wanafahamu. Samaki huyu sasa hivi inakadiriwa kwamba kwa kina chetu cha bahari ya hindi wako samaki milioni 50. Katika hao samaki wanavuliwa na meli zinazotoka nje ya Tanzania na samaki hawa wana uwezo wa kutaga mayai mmoja mmoja milioni moja moja kila samaki huyu mmoja, tafsiri yake ukizidisha hesabu rahisi tu pale, maana yake ni milioni 50, ukizidisha kwa samaki hao milioni 50 na kwa mayai milioni moja moja unaweza ukapata zaidi ya trilioni 50 mayai ambayo yanaweza yakatagwa ama vifaranga katika huo uchumi wa bahari kuu. Tafsiri yake nyingine pia ni kwamba kwa miezi mitatu baada ya kutagwa mayai samaki huyu anakuwa na urefu na uzito wa takribani kilo 10 mpaka kilo 20 na akizidi zaidi ya miezi minne mpaka mitano anakuwa na uzito wa takriban kilo 80 na maximum kabisa ni kilo 95. Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tuchukue tu hawa ambao wanakuwa na kilo 80; sasa kilo 80 kwa samaki mmoja ambaye anauzwa kwa dola za Kimarekani 18,000 kwa rate ya leo ya Kitanzania ya Sh.2,320, ni sawasawa na kusema samaki mmoja ana uwezo wa kuuzwa kwa Sh.41,760,000 za kitanzania. Huu ni uchumi mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukichukulia sasa hao samaki milioni 50 zidisha kwa samaki mmoja mwenye thamani ya Sh.41,760,000 ni zaidi ya trilioni mbili ambazo zilitakiwa ziingizwe kupitia uchumi wa bahari kuu. Hii hatuifanyi, hivyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Uvuvi na Mifugo asimamie hili na nitampa taarifa zote na ripoti zote ambazo zinaonesha ni kwa kiwango gani Tanzania tunaweza kufikia trilioni mbili kwa mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, tumezungumza hapa habari za elimu yetu ya Tanzania…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, nitaleta maandiko lakini nitachangia zaidi kwa suala la elimu ili tuone namna gani wenzetu wa South Africa wameweza kuepukana na suala hili zima la ajira kutumia mfumo wao unaoitwa YES. YES maana yake Youth Employment Service.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa fursa hii nami niweze kuchangia rasimu ya Mpango iliyowasilishwa hapa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Ni dhahiri kwamba, Waheshimiwa Wabunge wamechangia hapa, lakini nataka tu niweke kumbukumbu sawa hasa katika masuala haya ya mipango kwa maana ya tunapopanga, maana tunasema kupanga ni kuchagua, lakini mipango yote hii ni mizuri na Serikali yetu imeendelea kuitekeleza; mingine imetekelezeka, mingine bado.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nishauri katika eneo hili la Tume ya Mipango. Tunapopanga lazima tuwe na Tume ya Mipango iliyo imara sana. miaka ya nyuma kulikuwa kuna Wizara kabisa inayoshughulikia masuala haya ya mipango, sasa hivi Tume ya Mipango ni Idara ndani ya Wizara ya Fedha. Tafsiri yake ni kwamba, kama hakutakuwa kuna coordination, monitory and evaluation, tathmini na ufuatiliaji wa mipango yote tunayotaka kuipanga katika kipindi cha mwaka mmoja ama miaka mitano, itakuwa ni kazi bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwa Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tume ya Mipango ndio mpango mzima wa kutekeleza mipango hii ambayo tunategemea kuifanya. Kwa mfano mwaka 2010, mfano tu rahisi, Wizara ya Kilimo kipindi hicho pamoja na Wizara ya Maji walijenga vituo katika maeneo mengi nchini, zaidi ya vituo 200 na zaidi, hata kule jimboni kwangu kipo kimetumia zaidi ya milioni 900, hivi ninavyosema ni gofu, hakiendelezwi kiko vilevile tu. Maana yake thamani ya fedha iliyowekezwa pale haina tija kwa wananchi wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo lilikuwa zuri tu kwamba, wananchi itakuwa ni kituo cha kwenda kumwagilia pamoja na kujifunza mambo ya kilimo, lakini kimetelekezwa. Kimetelekezwa kwa sababu gani, hakuna muunganiko kati ya sekta moja na sekta nyingine ili kuishirikisha hiyo mipango na hatimaye iwe endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nichangie ni suala la elimu yetu ya Tanzania. Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa elimu yetu ya Tanzania asilimia kubwa ni theory zaidi na sio practical kuanzia chekechea mpaka chuo kikuu. Naweza nikatoa mfano rahisi tu, kuna mwenzangu mmoja ambaye nilisoma naye zamani, tulikuwa tunasoma computer science, lakini computer science hiyo computer yenyewe tumekuja kuiona mwaka wa tatu, ndio computer hata kuifungua, hebu imagine. Tafsiri yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake tulikuwa tunafanya ma-intergrations mengi, ma-theory, lakini practical ile yenyewe ile hatukuwa tunafanya. Kwa hiyo, niombe Wizara ya Elimu kwamba, sasa ni wakati wa kubadilisha mitaala yetu ya elimu. Ndio maana nchi zilizoendelea kama China wamewekeza sana katika ufundi na huku na sisi tumeanza kujenga vyuo vya ufundi ni jambo jema, lakini huko technicians wale ndio wataalam hasa. Hata akiwepo engineer mmoja, lakini technicians kwa wingi zaidi ndio mpango mzima kwa maana ya kutekeleza yale ambayo tunategemea yawe. Kwa hiyo, mfumo wetu wa elimu kuna haja kubwa sana ya kufanya transformation, tusipofanya hivi hawatakuwepo watu wa kusimamia na ambaye atajituma. Maana kila mmoja ukiwa na degree unategemea atakuwa bosi wa nani juu ya nani? Sio rahisi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la mfumo wa elimu ndio linasababisha pia changamoto katika ajira kwa vijana. Kwa mfano South Africa wana mfumo mmoja unaitwa YES. YES tafsiri yake ni Youth Employment Service, una accommodate wanafunzi wote wanaomaliza vyuo vikuu na vyuo vya kati kwenda kwenye taasisi binafsi. Namna gani inafanya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko namna hii; Rais wa nchi ile Cecil Ramaphosa alipokuwa ameuzindua lengo lake kubwa ni kwamba, badala ya vijana katika matangazo mengi ya kazi ambayo yanahitaji pengine uzoefu wa miaka mitano, uzoefu wa miaka kumi na hawa ndio wametoka ku- graduate wametoa wapi huo uzoefu; kwa hiyo, ikabidi waanzishe mfumo ambao utakuwa rahisi kuwachomeka kama vile field wanapokwenda. Wanakwenda katika kampuni, wanakwenda katika taasisi, wanakwenda katika mashirika, lakini unaratibiwa na Serikali na Serikali kazi yake ni kuwezesha hizo kampuni ama hizo taasisi ama sekta binafsi, ili sasa wale vijana ambao wanakwenda kusoma kule au wanakwenda kujifunza kazi kule baada ya muda fulani watakuwa tayari wamepata experience na kazi inapotokea Serikalini ama binafsi wao wenyewe ndio watakaokuwa wa kwanza kuajiriwa badala ya hivi tulivyo kwa sasa kwa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda sio rafiki sana, lakini nitaandika kwa maandiko suala la uchumi wa kidigitali. Namna gani Tanzania tunaweza tukaneemeka na uchumi wa kidigitali. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia katika Ofisi hii ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Kabla ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, ambaye ametujalia uzima hata leo tukawa kwenye Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze sana, nikianza na Mheshimiwa Waziri mwenyewe, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu pamoja na watendaji wote wa Wizara hii ya TAMISEMI, kwa sababu wanaitendea haki Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wenzangu wengi wamezungumza habari za TARURA. Ni kweli TARURA ndiye mkombozi mkubwa kwa sekta ya uchukuzi na mawasiliano katika maeneo yote vijijini na asilimia kubwa ya Waheshimiwa Wabunge hapa tunatoka majimbo ya vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichangie kuhusu TARURA kwa sababu kwanza kwa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, amesema TARURA ina kilometa 108,946, lakini fedha wanayopata TARURA kwa mwaka wa 2021 ni shilingi bilioni 275.03, sawasawa na asilimia 35 tu ya uhitaji wa bajeti nzima ya TARURA. Ili TARURA iweze kusimama, lazima iwe na zaidi ya shilingi bilioni 700 ambapo tunaweza tukakarabati kilometa hizi 108,946. Kwa bahati mbaya sana, fedha zinazotolewa hadi sasa zimetolewa bilioni 172.85, sawa na asilimia 63 ya fedha zote bilioni 275 na bado kuna utofauti wa bilioni 102.8. Kwa vyovyote vile kwa hali ilivyo katika majimbo yetu mengi vijijini hayapitiki na ni mvua zinaponyesha sana kila sehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niiombe sana Wizara, Mheshimiwa Waziri pamoja na Serikali nzima, ione umuhimu wa kuongeza fedha katika sekta hii ya TARURA. Watendaji wake wote wanafanya kazi nzuri sana akiwemo CEO wao pamoja na watendaji wengine, licha ya kwamba kuna upungufu mdogomdogo ambayo mimi naweza nikayasema. Kwa mfano, maamuzi mengi yanafanyika mikoani, tunatamani ifanyike transformation TARURA, kwamba badala ya maamuzi mengi kufanyika mikoani, basi yafanyike ngazi ya halmashauri, ngazi ya wilaya ambako ndiko wataalam wapo. Kwa sababu sasa hivi barabara nyingi zinaharibika vijijini, lakini anayefanya maamuzi yuko mkoani ambapo mkoani kule barabara ni nzuri. Kwa hiyo kunakuwa kuna delaying technique ya kufanya barabara hizi zisitengenezeke kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano rahisi tu ni Jimbo langu la Busokelo. Busokelo kule mvua tunapata kwa mwaka mzima, zaidi ya milimita 2,000 kila mwaka, tunapumzika mwezi Septemba pekee. Ukipumzika mwezi Septemba tafsiri yake bajeti tunazopitisha hapa Bungeni, tarehe Mosi, Julai zinatakiwa zianze kutangazwa tenda, lakini zinakuja kutangazwa mpaka mwezi Novemba ama Desemba. Kwa hiyo utakuta kipindi cha kufanya procurement system zozote zinakuwa ni muda mrefu sana na wakati utekelezaji wake unakuwa kipindi cha masika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana mara tu Bunge likipitisha fedha za Serikali, manunuzi yaanze mara moja badala ya kusubiri kufikia mwezi Desemba ama Januari ambapo barabara nyingi zinakuwa zimeharibika na zinakuwa zimekata mawasiliano katika kata mbalimbali, kitu ambacho hakikubaliki kwa ulimwengu wa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukizungumzia TARURA unazungumzia pia mifumo inayotumika katika manunuzi. Kuna Mfumo mmoja unaitwa TANePS, huu mfumo umekuwa ni changamoto kubwa sana, unasimamiwa na TCRA. Unaweza ukasajili wewe mkandarasi ama Engineers ambao wanakuwa kwenye huo mfumo, lakini matokeo yake baadhi ya passwords, tenda na documents kwenye huo mfumo, zinapotea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo utakuta inachukua muda mrefu sana mpaka tena huo mfumo usimame ili kuweza ku-process manunuzi hayo. Kwa hiyo nitoe wito na ushauri kwa Serikali kwamba kama inawezekana huu mfumo uweze kuwa revised badala ya jinsi ulivyo hivi sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara moja kwa wastani ni kati ya shilingi milioni 25 mpaka milioni 30, lakini kwa sasa barabara moja ya TARURA inatengenezwa kwa shilingi 2,524,461 kwa kilometa, hiyo ni shilingi lakini kwa kilometa moja. Wakati wenzetu wa Road Fund kupitia TANROADS wao ni zaidi ya fedha hizi. Kwa vyovyote barabara zetu hazitaweza kutengenezeka vyema kwa uwiano huu ambao tuko nao mpaka leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo kubwa lililopo hapa tuna kitu tunaita data backlog maintenance, maana yake inahitaji barabara nyingi zitengenezwe kipindi cha mvua, kitu ambacho siyo rahisi. Kwa hiyo inabidi zitengenezwe kipindi ambacho siyo cha mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kupitia TARURA hii kuna asilimia 30 ambazo Waheshimiwa Wabunge inawezekana wengi tunafahamu, wengine hatufahamu, ambazo ni maalum kwa vikundi, tunaita special groups, maana yake vijana, wenye ulemavu, wazee na wanawake ambayo kila bajeti ya TARURA lazima kuwe na asilimia hizo 30, lakini ni halmashauri chache sana zinazotenga fedha hizi ili kuviwezesha hivyo vikundi kupata fedha, lakini si tu kupata fedha, vifanye kazi za TARURA kwa asilimia 30. Kwa hiyo nisisitize kwa Mheshimiwa Waziri kwamba hili pia ni muhimu kulisimamia katika Wizara yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TAMISEMI ina mifumo mingi sana. Nilikuwa naorodhesha mifumo hapa, iko zaidi ya mifumo 14 na mifumo yote hii inaisaidia TAMISEMI. Hata hivyo, mifumo hii haitakuwa na maana sana kama gharama za kiuendeshaji zinakuwa kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niishauri Wizara kwamba kuna haja ya kupunguza mifumo ambayo iko TAMISEMI na wakati mwingine inakuwa ni redundant kwa maana kwamba mingine haifanyi kazi ipasavyo. Kuna kila sababu ya kuanzisha mfumo ambao uta-integrate na hii mifumo iongee, iwasiliane, ndipo tutakapoona haja ya kuwa na mifumo hii. Kwa hivi sasa ilivyo ni mifumo mingi sana na inatengeneza gharama kubwa kwa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza habari za TARURA, wamezungumza habari za malipo kuchelewa, wamezungumza habari nyingi, lakini tukiwa na mfumo mmoja ambao huo utakuwa chini ya Kitengo cha Monitoring and Evaluation, maana yake M&E ambao kila bajeti tunazopitisha hapa utakuwa na component ya kila mradi.

Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge popote utakapokuwa, awe kiongozi yeyote ngazi ya wilaya ama mkoa ama Taifa, una uwezo wa ku-trace back mradi wako na hata ukajua progress, ukajua kama bajeti imetolewa ama haijatolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii hatuna mifumo hii ndiyo maana CAG anapokuja na taarifa zake utakuta fedha nyingi zimeshapotea wakati tulikuwa na uwezo wa kufanya monitoring and evaluation kwa maana ya ufuatiliaji na tathmini kabla fedha hizi hazijatolewa. Nitoe wito, kwa sababu monitoring and evaluation kila mradi ukiwa nayo, hakika tutafikia malengo yetu kama Wabunge. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehma ambaye ametufanya tuwepo katika Bunge lako hili Tukufu. Pili, nimpongeze sana Waziri wa Elimu, Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako kwa kuiongoza vizuri Wizara hii ya Elimu pamoja na Naibu wake na watendaji wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa, nimshukuru Mheshimiwa Waziri na Serikali yote ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo wameweza kulitendea haki Jimbo la Busokelo. Busokelo mengi yamefanyika kupitia Wizara ya Mheshimiwa Prof. Ndalichako hususan ujenzi wa shule mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyozungumza katika Mkoa wa Mbeya mojawapo ya halmashauri zinazofanya vizuri sana kwenye mitihani ya kidato cha nne Busokelo tumekuwa tukiongoza kwa miaka miwili mfululizo. Hii ni kutokana na msaada mliotupatia kama wa ujenzi wa shule za wasichana na za watoto wa kiume. Kwa mfano, Busokelo Girls imejengwa na inafanya vizuri na ndiyo inayoongoza, Busokelo Boys imejengwa inafanya vizuri na inaongoza. Kuna shule nyingine zimekarabatiwa kama Ntaba Sekondari, Mwakaleli Sekondari, Ruangwa, Lufilyo, kwa kweli mnastahiki pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zaidi ya yote mmejenga na Chuo cha VETA ambapo leo hii VETA Busokelo inachukua wanafunzi kutoka mikoa mbalimbali. Niipongeze sana Wizara hii kwa sababu hivi karibuni walitoa agizo kwamba vyuo vyote vya VETA vichukue wanafunzi na ambao siyo wanafunzi waende kusoma katika vyuo vyote nchini. Busokelo tumelitekeleza hilo na hadi sasa wameshajiandikisha zaidi ya wanafunzi 300. Kwa hiyo, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu na kwenye Vitabu vya Imani mfano Biblia imesema: “Mkamate sana elimu, usimwache aende zake; Mshike, maana yeye ni uzima wako”. Maneno haya ni kutoka Mithali 4:13 ndiyo maana tunang’ang’ana na suala zima la elimu. Mataifa mengi yaliyoendelea yamewekeza sana kwenye sekta ya elimu. Ni- compliment michango ya Waheshimiwa Wabunge kwamba Taifa kama China waliwekeza sana katika ufundi ama vyuo vya kati ndiyo maana leo hii ipo vile ambavyo tunaiona. Hawakuwekeza sana katika vyuo vikuu kwa sababu waliona wafanyakazi wazuri ni wale ambao wamepata elimu ya kati ama vyuo vya kati. Kwa hiyo, naamini pia tunaweza tukajifunza kupitia kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi inayoongoza kwa kutoa elimu bora dunia nzima ni Finland. Pia tunaweza tukapeleka wataalam wetu huko wakajifunza kwa nini Finland inaongoza kwa kutoa elimu bora. Ukisoma ripoti mbalimbali za World Economic Forum pamoja na ripoti zingine utaona hiki nachozungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri yafuatayo katika sekta ya elimu. Tumezungumza suala la mitaala, ni kweli ni changamoto na Mheshimiwa Waziri ametoa commitment hapa kwamba wanakwenda kuibadilisha ama kuihusisha mitaala hii ya elimu. Ikimpendeza Mheshimiwa Waziri anaweza kutuma wataalam wake ama wao wakaja huku wenzetu wa South Africa, wana mfumo ambao nimewahiusema huku Bungeni ambao unawasadia sana vijana wengi ambao wanamaliza vyuo na wengine wakiwa vyuoni kupata kazi baada ya kumaliza masomo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, wao wanatumia mfumo unaitwa Youth Education System (YES). Tafsiri yake hawataishia tu kwamba wakisoma imetoka lakini Serikali inafanya utaratibu mara baada ya kumaliza masomo yao ya vyuo kuwaunganisha na taasisi, mashirika na makampuni mbalimbali yaliyopo katika nchi yao. Sisi pia tukifanya hivyo maana yake wanapotoka kule wanakuwa na ujuzi kamili kwa sababu kwa miaka hii mitatu mwanafunzi akiwa chuoni siyo rahisi sana kupata uzoefu wa kusema anaweza kufanya kazi bali akiunganishwa na taasisi na mashirika ambayo yanafanya kazi tayari itakuwa rahisi sana huyo mwanafunzi kupata ujuzi lakini baadaye kuajiriwa na taasisi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili nataka nizungumzie suala la Bodi ya Mikopo. Nimezungumza hapa mara nyingi na tarehe 31 Machi, 2021 niliuliza swali, je, ni sifa zipi za mwanafunzi ambaye anastahili kupata mikopo? Mheshimiwa Naibu Waziri alieleza lakini ukweli Bodi ya Mikopo kuna haja ya msingi ya kufanya either transformation ama kubadilisha kanuni zinginezo ili wanafunzi wote wenye sifa wapate mikopo siyo kama ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni miongoni mwa Wabunge ambao nimewapeleka wanafunzi wangu zaidi ya 20, zaidi ya mara mbili au mara tatu kwenda Dar es Salaam kuwatafutia mikopo maana wana sifa lakini hawapewi mikopo. Ukikutana na Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Mikopo atakwambia vizuri kabisa lakini utekelezaji wake unakuwa haupo. Nashauri Mheshimiwa Waziri aiangalie vyema hii Bodi ya Mikopo kwamba kuna haja ya msingi ya kubadilisha mifumo inayotumika pale ama kuiboresha zaidi ili wanafunzi wote wenye sifa wapate mikopo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na Mheshimiwa Mbunge aliyechangia jana mikopo hii isiwe tu kwa vyuo vikuu. Tumezungumza hapa kwamba nguvu kazi kubwa ipo katika vyuo vya kati, kama tutaweza kutoa mikopo hata kwa vyuo vya kati ndiyo tutapata nguvu kazi ya kuzalisha lakini uchumi utaboreka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kuzungumzia ni suala zima la upungufu wa walimu katika shule na halmshauri zetu. Busokelo peke yake walimu wa sekondari kuna upungufu wa zaidi ya walimu 93, walimu wa shule za msingi 439 pamoja na matundu ya vyoo zaidi ya 500. Kwa hiyo, tunawaomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja ku-wind up hapa aone namna gani anaweza kutusaidia katika jimbo hili la Busokelo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunajenga shule nyingine kwa kushirikiana na wananchi wa Busokelo, kuna shule inaitwa Kifunda Sekondari, Ntaba Sekondari na Ndembo Sekondari. Pia nitumie fursa hii kuwapongeza sana Diaspora wa Busokelo ambao wameendelea kuiwezesha na kuichangia shule yetu ya sekondari inayoitwa Busokelo Girls. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na hayo nataka nimalizie kwa kusema, tukiboresha vyuo vya VETA kwa maana ya vyuo vya ufundi, nina hakika elimu yetu ya Tanzania na ajira hakutakuwa na changamoto kwa kuwa watakuwa wamepata ujuzi hakika na sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkongo hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi kwa kunipa fursa niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi.

Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametufanya leo tuwepo asubuhi hii, na kipekee nikushukuru wewe namna ambavyo unaongoza Bunge lako zuri na zaidi pia niishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Waziri Mheshimiwa Mashimba Ndaki, pamoja na Naibu Waziri - Mheshimiwa Ulega. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nataka nichangie katika maeneo mawili ya uvuvi pamoja na ufugaji hususan katika Jimbo la Busokelo, lakini kabla sijafika huko ningeanza kwanza kwa kuishukuru Wizara mmetujengea majosho, mmetununulia majokofu ya chanjo, mmeanzisha mfumo ambao utatumika kwa wafugaji wote kwa ajili ya kuripoti maradhi yote ya wanyama kupitia mfumo huu najua Serikali itakuwa inapata taarifa sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na malalamiko na kilio cha wavuvi kwa muda mrefu hususan suala la nyavu. Siku za nyuma Serikali ilikuwa ikichoma nyavu ambazo hazijakidhi vigezo, lakini kwa bahati mbaya sana kulikuwa hamna uhalali ama uhalisia kwa nini wanachoma nyavu ambazo kimsingi kulikuwa kuna contradiction ama muingiliano wa kati ya Wizara pamoja na TBS. TBS wao wanatambua nyavu za milimita sita, lakini Wizara inatambua nyavu za milimita nane. Kwa hiyo, hawa watu wa Wizara wakienda kukamata nyavu kwa wavuvi wanaona hazijakidhi vigezo, lakini wakati huo yule anayetengeneza ama kutoka kiwandani China kwa nje ya box anaandika milimita nane, lakini kiuhalisia ndani ya box hizo nyavu inakuwa ni milimita sita. Kwa hiyo, ni hasara kubwa ambayo imetokana na kutokuwa na mahusiano kati ya Wizara pamoja na TBS ambavyo vyote viko chini ya Serikali. Nafikiri kuna haja ya jambo hili kuliweka vizuri ili tusiwatie hasara wavuvi wetu wakati ni makosa yetu sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka pia nichangie suala la uvuvi wa bahari kuu; kwenye Mpango wa Serikali mwezi wa pili nilichangia namna ambavyo bahari kuu (blue zone) inaweza ikaleta fedha nyingi sana katika pato la Taifa na niipongeze sana Serikali kwa kuchukua hatua madhubuti na wewe mwenyewe mwaka 2018 Bunge lako lilipounda Tume Maalum ya Masuala ya Uvuvi ilikuja na ripoti nzuri na ndiyo maana matokeo yake hivi leo Serikali imeamua kwenda kununua meli za uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze sana katika jambo hili sina sababu ya kurudia tena takwimu hizo kwa sababu tayari ninaamini Serikali mnakwenda kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nichangie kwenye ng’ombe wa maziwa; Jimbo langu la Busokelo tunazalisha maziwa mengi sana na maziwa mengi sana yanapotea na kwa bahati mbaya sana nchi tunaagiza tena maziwa kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, nataka nikupe taarifa takwimu zifuatazo; kwanza tuna ng’ombe 31,079; lakini kwa siku tunazalisha lita 124,320; kwa mwezi tunazalisha lita 3,729,600 ambapo kwa mwaka sawa na lita 44,755,200. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini bei ya maziwa yanayozalishwa Busokelo kwa lita ni shilingi 600 na kwa bahati mbaya sana maziwa ambayo yanaingia sokoni kwa ajili ya kununuliwa kwa siku ni lita 5,000 kutoka lita 124,320 yanayonunuliwa pekee ni lita 5000 wakati kwa mwezi yananunuliwa pekee ni lita 150,000 kutoka lita 3,729,600 na kwa mwaka maziwa yanayonunuliwa ni lita 1,800,000 kutoka lita 44,755,200 sawa sawa na kusema tunapoteza kwa mwaka fedha za Kitanzania shilingi 25,773,120,000 ni fedha nyingi sana hizi.

Sasa swali ambalo Waziri uje uwaambie wananchi wa Busokelo na Watanzania; kwa nini tunaagiza maziwa kutoka nje ya Tanzania angali maziwa lita zaidi ya 42,955,200 zinazalishwa Busokelo kupitia njia ya zero grazing? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaamini Waziri utakuja na majawabu sawasawa ili tusiendelee kuagiza maziwa nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda niunge mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia katika mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa. Awali ya yote nianze kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametufanya tuwepo hapa. Pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayowafanyia Watanzania wote. Tatu, nikupongeze wewe Mheshimiwa Spika kwa namna ambavyo unaongoza Bunge hili kwa viwango hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengi yamejadiliwa na Waheshimiwa Wabunge, nami niungane nao kwanza kwa kukubali mapendekezo ambayo wamependekeza katika Mpango huu hususani katika Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamezungumzwa, suala la Bandari, Reli, TAZARA, Meli, Barabara na Miundombinu yote yamezungumzwa. Aidha, nianze kwanza na Bandari ya Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bandari ya Tanga kwa historia ilianzishwa tangu mwaka 1888 lakini mwaka 1891 ndipo ilipokamilika. Kulikuwa kuna changamoto za uendeshaji na ujenzi wa Bandari hii, ndipo Serikali ilipoamua kwamba tuiboreshe Bandari hii ya Tanga. Ilifanyika katika awamu mbili na awamu ya kwanza, ilikuwa ni kufanya dragging kutoka kwenye kina kirefu umbali wa kilometa 1.7 mpaka kwenye gati. Awamu ya pili, ilikuwa ni kwa ajili ya kujenga gati mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe ufafanuzi hapa kwa sababu kumekuwa na sintofahamu ya kuelewa kwamba kilometa 1.7 ya dragging kwa maana ya kuchimba kile kina iko katika awamu gani katika miradi hii yote miwili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya kwanza, ilihusisha ujenzi huo na kuchimba kina kutoka mita tatu mpaka mita 13 ili meli kubwa ziweze kupita na kufika kwenye gati ama Bandari yenyewe ya Tanga. Kwa bahati nzuri mradi huu ulianza mwaka 2019 na umekamilika tayari kwa 100% na thamani ya mradi huu ilikuwa ni bilioni 172.3.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya pili, ilikuwa ni kwa ajili ya kujenga gati mbili na hizo gati ni awamu ambayo imeanza mwaka Septemba, 2020 na thamani ya mradi kwa awamu ya pili ilikuwa ni kiasi cha silingi bilioni 256.8. Kwa awamu hii mradi huu una asilimia 79 maana yake Mkandarasi bado yupo site. Nimeona nitoe ufafanuzi huu ili ieleweke kwa Watanzania wote na Bunge kwa sababu kulikuwa na mkanganyiko wa taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nilitolee ufafanuzi ni suala la Viwanja vya Ndege Nchini. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia kwamba ndege hazitui usiku, ni kweli Ndege hazitui kwa sababu viwanja vichache ndio vyenye taa. Tuna Kiwanja cha Mwalimu Nyerere kina taa, Songwe, Zanzibar na Mwanza. Katika mpango huu ambao sasa hivi Serikali imewekeza, tunakwenda kujenga viwanja vya ndege visivyopungua nane na tunakwenda kuweka na taa za kuongozea ndege usiku na mchana kikiwepo kiwanja chetu cha hapa Dodoma. Waheshimiwa Wabunge ninyi ni mashahidi kwamba kiwanja chetu hiki hakina taa na ndio maana ndege haiwezi kutua usiku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tulilazimika kuendelea kukijenga kiwanja hiki na kukiboresha kutokana na kwamba Kiwanja kipya cha Ndege cha Msalato ambacho hivi karibuni Mheshimiwa Rais ameshuhudia utiaji saini wa zaidi ya shilingi bilioni 360 kitakamilika mpaka 2024/2025. Tukaona kwa sababu Serikali tayari imekwishahamia Dodoma, kulikuwa kuna hoja kwamba kwa nini hatukuona kwamba kuna umuhimu wa kukiacha vile vile tusubiri hiki Kiwanja cha Msalato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba tumeona umuhimu wa kuboresha kiwanja hiki kwa sababu hapa ndipo Makao Makuu ya nchi, hapa ndio Makao Makuu ya Serikali na hapa ndio Makao Makuu ya Chama Tawala. Tukiwa na viwanja viwili katika mataifa mengine ndivyo wanavyofanya kwa maana ya kwamba hata kukiwa na emergence landing, inakuwa ni rahisi, inaweza kuwa kukawa na changamoto Kiwanja cha Msalato ndege ikatua hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja huu tayari tumekwishasaini zaidi ya Sh.6,438,450,107/= kwa ajili ya ujenzi wa taa na Mkandarasi ataanza kazi mara moja ambaye anaitwa Jess Espaňiola ambaye ataanza wakati wowote katika Kiwanja chetu cha Dodoma. Vile vile kuna viwanja vingine ambavyo vinaendelea na ujenzi kuna Kiwanja cha Songwe ambacho karibia kina kamilika, Kiwanja cha Songea, Mtwara, Iringa, Manyara ambacho pia tutaanza, kuna Kiwanja cha Kigoma, Tabora, Shinyanga na maeneo mengine mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ligine ambalo limezungumzwa sana hapa ni suala la ATCL kwamba ndege hazitoshi. Ni kweli hazitoshi, lakini katika Mpango huu Mheshimiwa Rais ametuagiza Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kununua ndege tano mpya ikiwemo ndege ya mizigo ambayo itaingia nchini mwakani mwezi Machi.

Kwa hiyo tutakuwa na ndege 16 zaidi, kwa hiyo hata kwa hizi changamoto za route ambazo zinatokea sasa hivi kutokana na kwamba ndege ni chache, ikitokea tu hitilafu kidogo maana yake hiyo route inaharibu route nzima. Sasa zikiingia Ndege hizi tano katika Mpango huu ambao Waheshimiwa Wabunge wamependekeza nina hakika suala la usafiri wa anga litakwenda kuimarika zaidi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda naunga mkono hoja hii ya Mpango na yale yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa tunakwenda kuyaweka na hasa ambayo hayakuwepo. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia kwenye Kamati zetu hizi zote mbili. Niwapongeze Waheshimiwa Wabunge wa Kamati hizi pamoja na Wenyeviti wote ambao wamewasilisha hoja iliyoko Mezani.

Mheshimiwa Spika, niungane na Waheshimiwa Wabunge kuishukuru sana Kamati ya Miundombinu ambao wamekuwa wakitoa kila mara ushauri katika Wizara yetu hii ya Ujenzi na Uchukuzi na wamekuwa msaada mkubwa katika mambo mengi. Nataka nifafanue zaidi hususan katika reli yetu ya SGR ambayo imeelezewa humu ndani, nataka niweke kumbukumbu sawa.

Mheshimiwa Spika, reli yetu ya SGR tangu imeanza kujengwa tulitangaza lot ya kwanza kutoka Dar-es- Salaam mpaka Morogoro. Kwa bahati mbaya waliorudisha tenda walikuwa ni wawili na hatimaye mmoja akajitoa akabakia mmoja, kwa hiyo, ikabidi afanye kazi hiyo mkandarasi mmoja. Kutoka Morogoro mpaka Makutupora ilipotangazwa alitokea mmoja, ikabidi apewe huyo huyo mmoja, lakini baada ya ku- bargain naye ama baada ya kupunguziana bei na lot iliyofuata ya Tabora – Isaka alitokea mmoja na akapewa kazi huyo huyo mmoja. Isaka – Mwanza walitokea wakandarasi wawili, aliyeshinda ndiye aliyepewa hiyo kazi.

Mheshimiwa Spika, sasa trend hii inaonesha nini? Kwa maana nyingine katika tenda zote ambazo kwa mujibu wa Sheria ya Manunuzi zimeainishwa, kuna tenda za aina nyingi, kuna competitive tender, kuna single source tender na zote ni njia sahihi ya kupata wakandarasi. Kwa hiyo, hakuna njia iliyo bora zaidi ya nyingine. Kwa hiyo, single source na ndio maana alivyokuwa anatokea mmoja huku tulikuwa tunam-award kwa sababu alikuwa amekidhi vigezo na Serikali tukawa tuimeridhia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niweke kumbukumbu sawa katika gharama za Mradi wa kutoka Tabora kwenda Kigoma pamoja Mradi kutoka Isaka kwenda Mwanza. Kwanza Mradi wa Isaka – Mwanza ulisainiwa Januari, 2021 kabla hata vita ya Ukraine na Russia, kwa maana nyingine kabla ya gharama kubwa kuongezeka. Mradi wa kutoka Tabora kwenda Kigoma umesainiwa tukiwa ndani ya vita ya Ukraine na Russia ambapo gharama za vifaa zimekuwa gharama kubwa sana, kwa vyovyote vile gharama yake itakuwa iko tofauti na mradi ule ambao ulisainiwa kabla ya dunia kuingia katika changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, gharama ya mradi wa Mwanza – Isaka ulikuwa Dola za Kimarekani pamoja na VAT, Dola za Kimarekani 1,123,794,312 hii pasipo VAT. Mradi ukiwa na VAT ulikuwa Dola 1,326,077,288 na gharama ya kilometa moja pasipo VAT, exclusive VAT, ni Dola za Kimarekani 3,295,584 na senti 49 na pamoja na VAT inakuwa Dola za Kimarekani kwa maana ya gharama ya kilometa moja 3,888,789 na senti 70. Huu ni Mradi wa Mwanza – isaka.

Mheshimiwa Spika, ukija Mradi wa Tabora – Kigoma; wote gharama yake pamoja na VAT ni Dola za Kimarekani 2,743,748,828 pamoja na VAT, pasipo VAT Dola za Kimarekani 2,325,210,871. Gharama kwa kilometa kwa huu mradi ni Dola za Kimarekani 4,595,000, hiyo pasipo VAT, ikiwa na VAT inakwenda Dola za Kimarekani 5,422,000.

Mheshimiwa Spika, kwa nini kuna variation kidogo hapa? Kuna variation kwa sababu, mbalimbali; ya kwanza, kutoka Isaka kwenda Mwanza kule ni mteremko au terrain yake ni ndogo. Kutoka Tabora kwenda Kigoma kuna terrain ama kuna…

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, Sheria ya Manunuzi pamoja na Kanuni zake zimetoa exception ya kutumia njia ya manunuzi ya single source, ambapo hizo taratibu inatakiwa lazima uzikidhi ndiyo uende. Sasa kama ufafanuzi huo anaoutoa kwamba huku Mwanza - Isaka ilitangazwa competitive watu wakashindana, lakini ilipofika Tabora - Kigoma haikutangazwa, na Sheria ya Manunuzi imeweka utaratibu wa namna ya kushughulika na single source.

Mheshimiwa Spika, single source inatumika tu pale inapolazimu kutumika. Sasa ukieleza kwamba suala hili kwingine huko kote tulitangaza akawa mmoja, kwa nini Tabora – Kigoma haikutangazwa akawa mmoja? Kwa nini akachaguliwa mtu mmoja? (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, nakuongezea dakika moja. Kwanza taarifa hiyo ya Mheshimiwa Mpina unaipokea? Halafu umalizie mchango wako.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, kwanza taarifa yake siipokei kwa sababu nimeshamwonesha trend yote, kwamba kuna sehemu ambako miradi hii ilitangazwa, lakini akatokea mtu mmoja. Kwa hiyo, hata maeneo ya lot No. 3, na Na. 4, kwa sababu trend ilikuwa kutokea mtu mmoja duniani wakati tunatangaza katika competitive tender ikabidi tuendelee kumchukua huyo huyo pasipo kujali kwamba wapo wengine, kwa kuwa walikuwa hawatokei. Kwa hiyo, taarifa yake siipokei.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, nataka niweke kumbukumbu sawa katika Bunge lako kwamba kuwepo kwa mikataba hii ambayo ni fixed contract, maana yake haitakuwa na variation tena, tofauti na miradi mingine yoyote. Kwa lugha nyingine, hii fedha ambayo tumeingia mkataba hapa, haitabadilika mpaka mradi ukamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, nataka nisisitize kwamba tenda ya kutoka Tabora kwenda Kigoma imekuwa ni tenda sahihi na aliyepata amepata kiusahihi na ameanza kazi kuusahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Sawa. Sasa katika kuweka sawasawa hizo kumbukumbu ulizosema, maana yake hivi vipande vingine, tenda zilitangazwa, wale waliojitokeza ninyi mkawatazama mkampa aliyestahili. Hata mlikotangaza halafu akajitokeza mmoja ndiye aliyepewa. Kwa hiyo, ni sehemu moja tu ya kutoka Tabora kuelekea Kigoma ndiyo ambayo amepewa yule wa mwendelezo. Nimeelewa sawa sawa?

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, umeelewa sawa sawa, kwa sababu yule alikuwa tayari yuko site na tukawa tunaendelea na kazi. Kwa hiyo, tukaona ni bora pia huyu aendelee na kazi. Kwa sababu maeneo mengi tukitangaza walikuwa hawajitokezi katika competitive tender.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye hotuba yetu ya Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi. Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametujalia na kufika hapa katika Bunge lako hili Tukufu na zaidi ya yote ninamshukuru tena Mwenyezi Mungu kwa namna ya kipekee, kupitia mtumishi wake Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye aliniteua nimsaidie kwenye Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi sekta ya uchukuzi kama Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru wewe pia na nikupongeze sana kwa kuwa Spika, wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchaguliwa kwa asilimia 100. Zaidi pia nimshukuru Makamu wa Rais, Waziri Mkuu pamoja na Waziri wangu Profesa Mbarawa kwa namna ya kipekee umekuwa ukitusimamia kama Kaka, kama rafiki. Mimi na mwezangu pacha tuko tayari kufanya kazi utakayotutuma wakati wowote.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninawashukuru pia na kuwapongeza Makatibu Wakuu wote wawili pamoja na Wakuu wa Taasisi zote ambao wamekuwa msaada katika kufanyakazi kwetu na zaidi ya yote niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao mmeshiriki kwa namna moja ama nyingine kuchangia bajeti yetu ya Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi, Mungu awabariki sana.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja zilizo mbele yetu ni nyingi, lakini kabla sijaendelea, napenda niwashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Busokero ambao walinipa heshima ya kuwa mwakilishi wao na zaidi pia nimshukuru mke wangu, familia na leo niko na Waheshimiwa Madiwani, Baraza la Madiwani liko ndani ya ukumbi huu kushuhudia bajeti hii likiongozwa na Mwenyekiti wa Chama pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri na Mkurugenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bajeti hii imechangiwa na wengi, lakini mimi nitajikita zaidi katika Sekta ya Mamlaka ya Bandari nchini (TPA) pamoja na Kampuni ya Ndege nchini (ATCL), Mamlaka ya Viwanja nchini (TAA) na nyinginezo; TCAA, TMA, pamoja na TAZARA na LATRA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikianza na Mamlaka ya Bandari nchini (TPA). Bandari yetu ya Dar es Salaam ndiyo lango kuu la uchumi wa nchi yetu ya Tanzania. Zaidi ya asilimia 40 ya mapato yote yanayokusanywa na TRA yanatoka kwenye lango hili la Bandari ya Dar es Salaam. Kwa maana hiyo, niwapongeze pia viongozi wote nikianza na Mkurugenzi Mtendaji kwa Mamlaka ya Bandari nchini ambapo wameweza kukusanya fedha zaidi ya Shilingi bilioni 895 na tunatarajia watafikisha Shilingi trilioni moja kwa mwaka huu. Ni historia ambayo haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bandari yetu ya Dar es Salaam ilikuwa na bandari zipatazo 66, lakini chini ya uongozi wa Mheshimiwa Prof. Mbarawa, mwezi huu tumerasimisha bandari 20 na kufanya bandari 86 zikiwemo pamoja za pale Dar es Salaam. Zaidi ya yote pia tuna bandari bubu zisizopungua 693 na hii ni kazi ambayo tunaliomba Bunge lako litupitishie bajeti hii ili tuweze kuzirasimisha zikiwemo na zile bandari alizosema Mheshimiwa kutoka Mkoa wa Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa bandari yetu ni lango kuu la uchumi wa nchi yetu, lakini kwa kuwa wateja wetu wakubwa wanaopitisha mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam wanatoka nchi za Kongo, Zambia, Rwanda, Burundi, Uganda, Malawi, hatuna budi kuunganisha mawasiliano kati ya bandari yetu na reli zetu nchini.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa habari ya reli ya TAZARA na reli ya kati. Mpango wa Serikali ni kuhakikisha ya kwamba chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ambaye hadi sasa tumeshasaini mikataba zaidi ya trilioni 14 kwa ajili ya SGR tafsiri yake tunakwenda kukusanya ama kupeleka mizigo ndani ya nchi ya Kongo kama mkakati wetu wa biashara.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, tumekusudia kwenda kufungua ofisi za TPA katika hizi nchi jirani ikiwemo Uganda, Kongo, Malawi na Zambia ili wateja ambao wanapata usumbufu kwenda nchi jirani ama kwenda bandari nyingine tuwakamatishie huko huko kwa kushirikiana na balozi zetu za nchi hizo. Huo ndiyo mpango wetu wa mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia shehena ambayo imepita ama imetoka katika bandari zetu, Zambia tuna asilimia 40 pekee. Maana yake asilimia 60 inakwenda Beira na Durban Afrika Kusini. Ukienda DRC tuna asilimia 39 kwa shehena 2,357,886; pia ukienda Burundi tuna asilimia 99.9 ambayo ni shehena ya 507,000; ukienda Rwanda ni shehena ya 1,369,000 sawasawa na asilimia 91, maana yake 9% wanakwenda kwenye bandari nyingine; ukienda Uganda ni 2%. Hapa tuna kazi ya kufanya. Zaidi ya asilimia 98 wanakwenda bandari nyingine. Maana yake tunahitaji kukaza buti ili asilimia 98 hizi zije kwenye bandari yetu.

Mheshimiwa Spika, ukienda Malawi asilimia 53 sawa na shehena kiasi cha 471,085. Kwa hiyo, nikubaliane na Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika mamlaka ya bandari nchini kwamba lazima nguvu kubwa tupeleke huko kwa maana ya kutangaza bandari yetu na pia kuwe na mfungamanisho kati ya bandari pamoja na miundombinu ya kusafirishia mizigo kwenda nchi hizo jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamezungumza suala electronic single window system. Ni kweli pale bandarini tuna mfumo huu, lakini mfumo huo haufanyi vyema. Hivi sasa tuko katika mazungumzo na bandari zinazofanya kazi vizuri duniani kama T-World watakaofanya shughuli hii kwa maana ya ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na Serikali kupitia TPA inafanya mazungumzo na wawekezaji hawa DP-World kwa lengo la kuona uwezekano wa kuingia makubaliano uwendeshaji wa baadhi ya vitengo vya bandarini ili tufanye kama wanavyofanya wenzetu huko duniani.

Mheshimiwa Spika, nikihama kutoka bandarini, nije ATCL. Waheshimiwa Wabunge wamezungumza sana kuhusiana na kampuni yetu ya ndege hapa nchini, ni kweli Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan hivi sasa anavyosema ameshakutoa fedha kwa ajili ya kununua ndege zingine tano ambazo zitaongeza idadi kutoka 11 mpaka 16 hii itaongeza usafiri ndani ya nchi yetu na nje ya nchi yetu kwa hiyo niungane na Waheshimiwa Wabunge kwamba ATCL ni mkombozi kwetu lakini pia inarahisisha usafiri na sisi waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kwamba unapotaka kwenda Dar es Salaam, tunapotaka kwenda mkoa wowote hususan kama Mwanza Mbeya na maeneo mengine tunatumia ndege hii kurahisisha usafiri wetu sasa safari ambazo tutaanza kuzitumia hivi karibuni kwa sasa tunakwenda nchi za Burundi Uganda, Comoro, China, Zimbabwe, Mumbashi, Kongo, Lusaka, Ndola Zambia, India Pamoja na Kenya.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tutafungua ofisi zetu nyingine na siyo tu kufungua ofisi katika hizo nchi, lakini pia tutaanza kwenda kwa Waheshimiwa Wabunge katika maeneo mbalimbali hususani tutaanza kwenda pemba, tutaanza kwenda Mombasa, tutaanza kwenda Musoma, maeneo yote ambayo viwanja sasa hivi vinajengwa na vinajengwa kwa sababu karibia tu tutaanza kwenda safari zetu za Air Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pia tutakwenda maeneo mengine kama London, tutakwenda Dubai, tutakwenda Johannesburg, tutakwenda Mayotte, tutakwenda Kinshansa, hizi nimeshazitaja Mombasa, Musoma Pamoja na Pemba.

Mheshimiwa Spika, waheshimiwa Wabunge pia wamezungumzia suala la fidia ni kweli kulikuwa na wafanyakazi katika shirika letu na makampuni yetu na ATCL lakini hivi ninavyosema zaidi ya Shilingi bilioni 131 zimekwishalipa kwa ajili ya wafanyakazi pamoja na kampuni ambazo zilikuwa zinaidai hii ATCL. Kwa maana hiyo, tunaomba Waheshimiwa Wabunge mtupitishie bajeti yetu ili twende kulipa madeni yaliyobaki ya kiasi cha Shilingi bilioni 5 kwenye kampuni yetu hii ya ndege.

Mheshimiwa Spika, najua ni mengi lakini niunge mkono hoja. Ahsante sana.