Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Eng. Hamad Yussuf Masauni (18 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Napenda kujibu baadhi ya hoja ambazo zimejitokeza kutoka kwa Kambi ya Upinzani na baadhi ya wachangiaji wa upande wa kule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza wanasema kwamba Serikali imeiweka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kijeshi, kimabavu na kwa kukiuka Katiba.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja hii naomba niigawe katika makundi mawili. Kuna hii dhana potofu ambayo imekuwa ikizungumzwa kwamba Serikali imepeleka maaskari wengi wakati wa uchaguzi Zanzibar, dhana ambayo siyo sahihi.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema siyo sahihi kwa sababu gani? Kwa mujibu wa taratibu za uchaguzi, mfano mdogo tu najaribu kutoa kwamba katika kila kituo cha uchaguzi inahitajika angalau wakae askari wawili na Zanzibar kuna vituo vya uchaguzi zaidi ya 1500. Kwa hiyo, ukichukua kwa kituo askari wawili maana yake unahitaji askari 3,000 na kati ya askari 5,000 walioko Zanzibar unabakiza askari 1,500 ambao hao hao wanahitajika kwa ajili ya mambo ya vital installation pamoja na misako, doria, kukaa standby, kufanya upelelezi na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashangaa uchaguzi ambao umefanyika tarehe 25 Oktoba upande wa Tanzania Bara kwa mfano tumetumia askari mpaka wa Zima Moto, JKT kwa sababu askari tuliokuwa nao hawatoshi. Takwimu zinaonyesha polisi mmoja anahudumia wastani wa wananchi 1,200. Kwa hiyo, kimsingi hili jambo linajaribu tu kuenezwa vibaya na hasa ukizingatia yale matishio ambayo yalikuwa yakienezwa ikiwemo ulipuaji wa mabomu, jitihada za kuchoma nyumba moto, kulikuwa kuna kila sababu ya Serikali kuwa makini sana katika kuhakikisha kwamba uchaguzi ule unakwenda kwa salama na amani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala ambalo linazungumzwa kwamba Katiba imekiukwa...
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kumwambia Mheshimiwa Rais Magufuli aingilie maamuzi ya ZEC na hoja ya kwamba vyombo vya ulinzi na usalama ambavyo viko kwenye Muungano kutekeleza jukumu la kikatiba kusimamia usalama wa raia na mali zake, hapo lipi ni kuvunja Katiba? Ni kumwambia Rais aingilie mamlaka ya ZEC ama polisi kuchukua kazi yake ya msingi ya kulinda raia na mali zao?
kuhakikisha kwamba uchaguzi wa marudio Zanzibar umekwenda kwa hali ya usalama na amani na Zanzibar na Tanzania kwa ujumla sasa hivi watu wanaishi vizuri, kwa salama na amani na watu wanafanya shughuli zao kama kawaida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, kuna hoja ambazo zimezungumzwa kwamba kuna watu wamekamatwakamatwa hovyo na sijui kuna watu wanaitwa mazombi, tumezungumza hapa kwenye Bunge kwamba sisi hatuwatambuwi. Tulichokisema na ambacho tunakirudia kusema hapa sasa hivi ni kwamba vyombo vya ulinzi vitatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa taratibu. Matukio ambayo yameripotiwa na ripoti hii ambayo inazungumzia matukio mengi sana ya uvunjifu wa Sheria za Uchaguzi yaliyosababisha Tume ikatoa maamuzi hayo na sisi tulichunguza. Kwa mfano, tulichunguza suala la kuzidi kwa kura ukilinganisha na wapiga kura, tumewabaini watu na ushahidi upo waliofanya matukio hayo.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la watu kuzuiliwa kupiga kura, watu Mawakala wa Vyama vya Siasa wamebururwa kama mbwa njiani, tumewabaini na tumewakamata, hakuna mtu aliyeripoti habari ya mazombi.
MBUNGE FULANI: Toa ushahidi.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Kuna suala la kufutwa kwa namba za matokeo kwenye fomu kwa makusudi kabisa, tumewabaini wahusika na wamekamatwa. Kuna takiribani watu zaidi ya 149 tumemaliza uchunguzi wao sasa uko kwa DPP, ni kazi ya DPP kuamua kuwapeleka mahakamani, sisi tumeshafanya kazi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengi yamefanyika ya ovyo kabisa katika uchaguzi halafu leo mtu anakuja hapa anasimama anasema uchaguzi ule.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumesema kwa mamlaka yetu tuhamishe vituo vya kuhesabia kura. Kuna vituo na majina naweza nikawatajia hapa, kituo kimoja kimetolewa Wawi kimepelekwa Chenjamjawiri, kweli si kweli? Akatae pale Mbunge Wawi, akatae!
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka niseme jambo moja kwamba suala la ulinzi na usalama katika nchi hii halina mjadala au mbadala. Leo hii nimesikia baadhi ya Wabunge wa upande wa kule wanataka kuleta vitisho. Mimi nataka nichukue fursa hii niseme hapa hapa Bungeni kwamba tunatoa onyo kali, kama wewe unaamua kutumia Bunge hili kuchochea vurugu hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria. Wale viongozi mnasema wamekamatwa iwe kiongozi wa chama chochote au raia, ikiwa wamekiuka sheria za nchi hii watakamatwa na watashughulikiwa kwa mujibu wa sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu niseme kwamba jukumu hilo ndiyo jukumu la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani na Jeshi la Polisi kuhakikisha kwamba tunasimamia usalama wa nchi hii. Niwapongeze sana Jeshi la Polisi kwa kazi nzuri sana waliyoifanya NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Kuna mtu anaitwa Pinde sijui ambaye ndiye alikuwa Msimamizi wa Uchaguzi amekiri mwenyewe kabisa kwamba alisimamia kinyume na sheria za uchaguzi. Sheria za Uchaguzi zinasema kura zihesabiwe kwenye kituo leo kiongozi ambaye amepewa mamlaka ya kusimamia uchaguzi Pemba anahalalisha uvunjifu wa sheria halafu sisi tusichungeze leo mnasema uchaguzi siyo huru na haki!
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nasema kwamba watu wote walioshikiliwa kwa kukiuka taratibu za uchaguzi kwa masuala ya jinai, polisi imeshafanya uchunguzi imeshaupeleka kwa DPP. Ni wajibu wa DPP, mahakama na mamlaka nyingine kuchukua hatua zinazostahili, sisi tumeshamaliza kazi yetu. Katika hilo hatutamstahi mtu yeyote iwe Mbunge, iwe mwanachama wa kawaida, iwe viongozi wa chama chochote anayekiuka sheria za nchi hii, sheria itafuata mkondo wake.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kwanza kumshukuru kabisa kwa dhati Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa imani kubwa aliyokuwa nayo kwangu na kuniteua kushika dhamana hii. Pia nimshukuru na Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vile vile nichukue fursa hii kuishukuru familia yangu na Mheshimiwa Waziri kwa jinsi ambavyo ananiongoza vizuri, nafanya nae kazi kwa karibu sana na pia kwa ushirikiano wa hali ya juu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukurani hizo, naomba sasa nichukue fursa hii kuweza kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizokuwa zimewasilishwa leo hii na Waheshimiwa Wabunge wa Bunge lako hili Tukufu. Naomba nianze na hii hoja ya makazi ya askari pamoja na vitendea kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja hii imezungumzwa ama imechangiwa kwa maandishi na kwa kuzungumza na wachangiaji wengi, lakini nitawataja wale ambao nimebahatika kuwabaini. Mheshimiwa Hamidu Bobali, Mheshimiwa Dkt. Shukuru Kawambwa, Mheshimiwa Kiula, Mheshimiwa Masare, Mheshimiwa Kigula, Mheshimiwa Kingu, Mheshimiwa Shekilindi, Mheshimiwa Komanya, Mheshimiwa Omari, Mheshimiwa Kangi Lugola na Mheshimiwa Kingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiofichika kwamba majeshi yote takribani yana changamoto kubwa sana ya makazi ya askari pamoja na vitendea kazi na kimekuwa hiki ni kilio cha Waheshimiwa Wabunge takribani cha muda mrefu. Tunakiri juu ya changamoto hii na ndiyo maana hivi tunavyozungumza, kuna mipango kabambe ya Serikali ambayo inalenga kuhakikisha kwamba inapunguza matatizo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Jeshi la Polisi, tayari kuna utaratibu wa kujenga nyumba takribani 4,136 ambapo zinatarajiwa kujengwa kupitia mkopo wa Serikali ya China kupitia EXIM BANK. Wakati huo huo kuna Ujenzi wa makazi ya nyumba za askari Mabatini-Mwanza ambao zinachukua familia 24, Buhekela - Kagera familia 12, Musoma - Mara familia 24, Ludewa - Njombe familia 12. Aidha, Serikali imejenga nyumba 22 za maafisa wa Mikocheni ambazo ziko Mikocheni na maghorofa 22 ambayo yatakuwa Kunduchi pale kwa ajili ya familia 333 za askari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa magereza, pia kuna mchakato wa kujenga nyumba takribani 9,500 lakini pia kwa upande wa vitendea kazi kwenye Jeshi la Polisi kuna mradi ambao programu ya kuleta magari 777 ya aina mbalimbali, miongoni mwao yameshaanza kufika na mengine yatakuja hatua kwa hatua, ni magari ya aina mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa upande wa Jeshi la Zimamoto katika bajeti yetu hii kwenye bajeti ya maendeleo tumetengewa takribani shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuongeza magari mawili ya kuzimia moto. Kwa hiyo, hizo ni miongoni mwa hatua ambazo tayari Serikali imeanza kuchukua kwa ajili ya kukabiliana na changamoto ya masuala haya ya vitendea kazi pamoja na makazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa kuna hoja ambayo imechangiwa na wajumbe wengi wakiwemo Mheshimiwa Mohamed Amour, Mheshimiwa Msigwa, Mheshimiwa Lwakatare, Mheshimiwa Kiula, Mheshimiwa Masoud, Mheshimiwa Yusuf, Mheshimiwa Mukasa, Mheshimiwa Kaiza, Mheshimiwa Anatropia na wengineo. Hoja hii zaidi ilikuwa inazungumzia kuhusiana na kubambikiwa kesi, wamelishutumu sana Jeshi la Polisi kwamba limekuwa likibambikia kesi, lakini nichukue fursa hii kuwapongeza Jeshi la Polisi kwa kazi nzuri ambayo wanafanya katika mazingira magumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya pongezi hizo ambazo nawapa Jeshi la Polisi, haiondoi ukweli kwamba kuna askari wachache sana, nasisitiza kwamba ni wachache sana ambao wamekuwa wakichafua taswira nzuri ya Jeshi la Polisi miongoni mwa wananchi na hatua nyingi zimechukuliwa katika kukabiliana na askari wa namna hii. Kuna mikakati ya kijumla na mikakati mingine ya mmoja mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati iko mingi, siwezi kuitaja yote, lakini wameweza kutoa mwongozo wa mara kwa mara kwa Wakuu wa vituo na Wakuu wa Upepelezi kuwa makini sana kwa majadiliano na mashauri yanayofunguliwa na kutoa maelekezo kwa wapelelezi wa kesi ambao watasaidia kufuatilia mwenendo wa kesi hizo. Pale ambapo askari wamegundulika kufanya matatizo kama hayo ya upendeleo, basi wamekuwa wakichukuliwa hatua za kinidhamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kesi moja ambayo inazungumzwa sana ambayo Mheshimiwa Kiula aliizungumza baada ya kufanya ziara ya Kamati katika gereza hapa Dodoma, lakini kesi hii hii na mimi naifahamu vizuri. Tumekuwa tuna utaratibu mzuri kupitia Mheshimiwa Waziri wangu, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kushirikiana na Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Mwakyembe kwa kufanya kazi kwa pamoja. Wakati huu niliweza kumwakilisha Mheshimiwa Waziri kufanya ziara katika lile gereza na kumshuhudia huyu msichana ambaye anazungumzwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli msichana huyu alikatwa vidole viwili vya miguu na viwili vya mikono na baada ya kukatwa vidole hivi vya mikono yeye ndiyo akafungwa miaka minne. Ni jambo ambalo linasikitisha sana. Hizi ziara tumekuwa tukizifanya katika maeneo mbalimbali tunapopata fursa, tumefanya katika magereza mengi ili kuweza kubaini kama kuna wananchi ambao wamekuwa wakibambikiziwa kesi ili hatua za haraka zichukuliwe na tumechukua hatua nyingi tu.
Katika hatua specific ambayo ameizungumza Mheshimiwa Kiula kwa huyu msichana ni kwamba, mpaka sasa hivi tunavyozungumza wale watu ambao walimkata kidole wameshafungwa, wamehukumiwa kufungwa nadhani miaka mitatu kama sikosei au minne tunavyozungumza sasa hivi. Pia ile kesi yake ambayo alibambikiwa ya kuvunja nyumba nayo imefutwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wale askari ambao walishiriki kwa namna moja ama nyingine kutomtendea haki huyu kijana tumeagiza wasimamishwe kazi mara moja na wachukuliwe hatua za kisheria. Kwa hiyo, kazi hii tumekuwa tukiifanya kimya kimya kuweza kutembelea kwenye magereza mbalimbali na kuweza kubaini watu ambao wanabambikiwa kesi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuhusiana na hoja hii malalamiko yamekuja upande wa masuala ya kisiasa. Mimi niseme tu kwamba Jeshi la Polisi linafanya kazi kwa mujibu wa sheria na taratibu. Katika kutimiza wajibu wake, wananchi tunapaswa kuwapa ushirikiano. Unapotakiwa na askari kutii lazima utii, wanaita sheria bila shuruti. Askari anapokuambia umefanya kosa fulani akakukamata basi ufuate sheria usilazimishe askari kutumia nguvu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya masuala yamezungumzwa sana lakini niseme kwamba Jeshi la Polisi limechukua hatua mbalimbali kulingana na taarifa ambazo imezipokea. Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakilalamika hapa mara nyingi kwamba kuna jambo fulani limetokea, lakini hakuna hatua iliyochukuliwa lakini ukimuuliza umepeleka taarifa hizo katika kituo gani cha polisi, hakuna. Kuna taarifa nyingi ambazo Jeshi la Polisi limezichukua na kuzifanyia kazi kwa sababu tuna lengo la kuhakikisha kwamba nchi yetu inaendelea kubakia katika amani na utulivu hasa kipindi cha uchaguzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi, mnakumbuka wakati wa uchaguzi hasa Zanzibar kuna matukio mengi ya uvunjifu wa amani yalikuwa yametokea. Kuna watu waliua wanyama, walichoma mashamba, walipiga nyumba alama ya “X”, wamechoma nyumba za watu, wamechoma maofisi ya vyama na wametega mabomu. Katika hali kama hii mnatarajia kwamba Jeshi la Polisi likae kimya? Ni Serikali gani ambayo itakubali amani ya nchi inachezewa halafu ikabakia kimya? Yaliyofanyika ni kuhakikisha kwa mujibu wa taarifa zilizopo na uchunguzi uliofanyika kuwakamata watuhumiwa mbalimbali, kufanya upelelezi na kuweza kuwafikisha panapostahiki na panapostahiki kwa mujibu wa sheria za nchi yetu ni kwa DPP ili baadaye waweze kupelekwa mahakamani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengi yamefanyika sina haja ya kuyarudia kuyazungumza hapa. Nashukuru leo hayajazunguzwa kama kipindi kilichopita lakini nilikuwa nimejiandaa kwelikweli maana nina ripoti ambayo ni very comprehensive ina ushahidi wa kila jambo ambalo limefanyika ambapo watu wanaolalamika humu ndani leo ndiyo wafuasi wao walikuwa mstari wa mbele kufanya mambo hayo, lakini leo wamekimbilia kwenye hoja nyingine. Mimi niseme tu kwamba tusaidiane, kama kuna mambo ambayo mnaona hayajachukuliwa hatua na ni matendo ya kihalifu yote yataweza kufanyiwa kazi ili mradi muwasilishe katika sehemu stahiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna jambo lingine limezungumzwa hili suala la mashehe. Wanasema kuna mashehe wamekamatwa kwa nini wanashtakiwa Dar es Salaam lakini kwa nini mashehe hawa wamedhalilishwa. Kwa ufupi kabisa kwa kuwa muda haupo, niseme tu kwamba mashehe hawa wameshtakiwa kwa makosa ya kigaidi…
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Makosa haya yamefanyika Tanzania Bara. Ndiyo maana walipokwenda kuhukumiwa Zanzibar wakasema haya makosa yamefanyika Tanzania Bara kwa hiyo wakaletwa Tanzania Bara kwa sababu ndiyo walifanyia huku makosa.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Sasa wanasema wamedhalilishwa, naomba niweke mezani ripoti hii ya uchunguzi ambapo walipelekwa hospitali, wakafanya uchunguzi hakuna hata mmoja alionekana ana uthibitisho wowote wa kudhalilishwa. Ripoti hii hapa naiweka mezani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie sasa katika hii hoja ya wahamiaji haramu ambapo wachangiaji wengi wamechangia lakini kutokana na muda naomba nisiwataje. Ni kweli tulifanya operesheni, ilikuwa ni operesheni kabambe ambayo ilianzia tarehe 24 Disemba mpaka tarehe 31 Januari. Katika operesheni hii tulifanya mambo kadhaa ikiwemo upelelezi, doria, misako, ukaguzi na kadhalika. Mafanikio tuliyoyapata ni makubwa sana ambapo takribani wahamiaji haramu 3,339 kutoka mataifa 33 wameweza kukamatwa. Aidha, hatua mbalimbali zimechukuliwa dhidi ya wahamiaji haramu hawa, wengine wamerudishwa majumbani kwao, wengine walikuwa wakimbizi wakarudishwa makambini, wengine wamepigwa PI Notice wameondoshwa, wengine wameamriwa kuondoka na wengine wanaendelea kuchunguzwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi hili lilikuwa na mafanikio makubwa kwani tumeweza kufanikiwa kukusanya takriban dola za Kimarekani laki moja na tisini na kitu elfu ambazo zilipatikana kupitia special visa kwa ajili ya wahamiaji haramu 317 ambao walikuwa wanaishi kinyemela. Vilevile zoezi limesaidia sana kuibua mwamko na hamasa kwa wananchi kuhusiana na madhara ya kukaa na wahamiaji haramu. Ndiyo maana tumeweza kupata karibu taarifa 750 kutoka kwa raia wema zilizoweza kusaidia kuwakamata hawa wahamiaji haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi wageni walio wengi wanafuata sheria na ndiyo maana tunasema kwamba baada ya operesheni hii kabambe tumekuwa na mfumo mzuri wa kuwashughulikia. Hivi ninavyozungumza nadhani kesho watendaji wa Idara ya Kazi watafika hapa na watendaji wetu wa Idara ya Uhamiaji wako hapa tutakaa pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kazi ili tuweze sasa kuwa na mkakati wa pamoja wa kufanya zoezi letu liwe endelevu. Mkakati huu utasaidia sana kuendeleza mafanikio makubwa ambayo tumeyapata.
Mheshimiwa Mweyekiti, kulikuwa na hoja nyingine ambayo inazungumzia hili suala la zimamoto. Wachangiaji wengi wamelalamika hapa kwamba mara nyingi moto unapotokea kwenye majengo marefu kikosi chetu hakina uwezo. Mheshimiwa Lucy Owenya alisisitiza sana hoja hii katika mchango wake wa maandishi na wachangiaji wengine walisisitiza kwamba unapotokea moto katika majengo marefu kikosi chetu cha zima moto hakina uwezo wa kuzima moto, ni kweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza kwa mujibu wa vitendea kazi ambavyo tunavyo, tuna gari ambayo yanaweza kufika mwisho ghorofa 18 na wakati sasa hivi tuna majengo yana mpaka ghorofa 17. Ndiyo maana tukasisitiza kwa mujibu wa sheria ya mwaka 2007 na kanuni zake ni lazima majengo mapya yatakayojengwa yazingatie usalama kwa kuweka vifaa vya kisasa ikiwemo automatic fire system na automatic fire detection and suppression system. Mfumo huu utasaidia sana kuweza kupunguza madhara yatakayoweza kutokea moto utakapotokea katika majengo ambayo ni marefu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo sasa hivi tunafanya jitihada za kuhakikisha kwamba tunapunguza madhara ya moto kwa kuongeza vifaa vya kuzimia moto. Juzi nilizungumza hapa kwamba miongoni mwa mambo ambayo tunajaribu kufanya ni kuhakikisha kwamba tunatumia magari yaliyokuwa ya washawasha, yale 32 ambayo yameingia pia yaweze kusaidia katika shughuli ya uzimaji moto.
Mheshimiwa Mwenyekiti naona nimetumia muda wangu vizuri, yale ambayo tumekubaliana niyazungumze nimeyazungumza. Naomba sasa nimuachie Mheshimiwa Waziri na yeye aweze kuendelea na pale ambapo mimi sikupagusa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nianze kutumia fursa hii kumshukuru sana kwa mara nyingine Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuendelea kuniamini kwenye majukumu haya muhimu. Naomba nitumie methali ya wahenga fupi tu ambayo inasema kwamba imani huzaa imani, mimi na Mheshimiwa Waziri ambaye kwa kweli amekuwa akinipa ushirikiano wa hali ya juu na msaada mkubwa sana katika kutekeleza majukumu yangu, tutaendelea kuchapa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu muhimu wengi kweli wa kuwashukuru lakini kwa kuwa muda ni mfupi, naomba moja kwa moja niende katika hoja za Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wamechangia mambo mengi sana, wengine kwa kuzungumza na wengine kwa maandishi. Kwa muda huu inawezekana siyo hoja zote za Waheshimiwa Wabunge tutakazoweza kuzipatia majibu, lakini zile ambazo hazitapatiwa majibu kwa njia ya kuzungumza tutawapatia majibu kwa njia ya maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hoja ya suala la usalama barabarani. Leo hii tunazungumzia changamoto ya usalama barabarani katika nchi yetu katika kipindi ambapo Taifa tumepata msiba mkubwa sana wa ajali ya basi lililojeruhi na kuua watoto na vijana wetu ambao walikuwa wana shughuli za masomo. Naomba Mwenyezi Mungu atupe moyo wa subira pamoja na wazazi wa watoto hawa katika kipindi hiki kigumu. Wakati tukiendelea kuomboleza msiba huu mzito, inaweza ikawa vigumu sana kueleza kwamba katika eneo hili la usalama barabarani tumefanya kazi kubwa sana katika kipindi cha mwaka mmoja na tumefanikiwa kwa kiwango cha kuridhisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufikisha azma yetu hii ya kupunguza ajali za barabarani kuna hatua kadhaa tulizichukua. Moja katika hatua ambazo tulichukua tulianzisha mkakati kabambe wa miezi sita ambao ulikuwa na lengo la kupunguza ajali za barabarani kwa asilimia kumi. Kiukweli mkakati huo umefanikiwa kwa kiasi cha kuridhisha ingawa tumegundua changamoto nyingine za hapa na pale ambazo tutazifanyia kazi. Mkakati huu ulizingatia mambo makubwa matatu ambayo ni vyanzo vya ajali barabarani ambavyo vinasababishwa na makosa ya kibinadamu, ambapo mara nyingi makosa haya yanatokana na uzembe wa madereva wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni kwa asilimia ndogo ni changamoto ya miundombinu yetu na changamoto ya ubovu wa magari. Kwa hiyo, mkakati wetu ambao ulilenga maeneo 14 zaidi uliangalia maeneo hayo matatu. Leo hii nimesimama hapa mbele yako na mbele ya Waheshimiwa Wabunge kuelezea tathmini kwa ufupi ya mafanikio hayo ambayo tulilenga kupunguza asilimia kumi ya ajali katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kukamilika kwa mkakati ule wa miezi sita tumefanikiwa kupunguza kwa upande wa ajali za magari ambazo zinasababisha madhara makubwa, tumefanikiwa kupunguza ajali za vifo kwa asilimia nane, hatukufikia asilimia kumi lakini tumekaribia, asilimia nane. Katika ajali za majeruhi tumevuka viwango na kufikia asilimia 13. Kwa upande wa pikipiki tumefanikiwa kupunguza ajali kwa asilimia 17 zile ajali ambazo zinasababisha vifo lakini kwa majeruhi wa pikipiki hatukufanya vizuri sana na ajali ziliongezeka kwa asilimia mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla ukiangalia utaona kwamba kwa kiwango kikubwa ajali hizi zimefanikiwa kupungua katika kipindi hiki cha miezi sita. Mkakati huo wa miezi sita ndiyo uliopelekea mafanikio ambayo leo hii tunajivunia kipindi cha mwaka mmoja wa kupunguza ajali kwa asilimia 7.2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto mbalimbali ambazo tunakabiliana nazo, najua eneo hili limeguswa na Waheshimiwa Wabunge wengi, nitawataja baadaye ambao wamechangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa changamoto ambazo tumekabiliana nazo kama ambavyo baadhi ya Wabunge waliochangia wamezungumza, moja ni changamoto ya sheria yetu tuliyonayo sasa hivi, ambapo baadhi ya mambo yanahitaji kufanyiwa marekebisho. Kuna mambo machache ambayo nitayataja kwa haraka. Kwanza kunahitajika kuongeza ukali wa adhabu katika sheria yetu, vilevile kunahitajika kuongeza idadi na aina ya makosa ambayo hayamo katika sheria ya sasa hivi. Kwa hiyo, katika mambo 14 ambayo tumeyaangalia moja lilikuwa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengine ambayo tumeyaangalia na Waheshimiwa Wabunge wameyazungumza kwa uchungu kabisa, kwamba kuna tatizo kuhusu Askari ya Barabarani, wengine wamefika mpaka kusema Askari wanakaa juu ya miti. Tuna changamoto moja ya kisheria, lakini kuna changamoto vilevile nyingine ya kimfumo wa nchi yetu. Tunapozungumza sasa hivi tunatumia mfumo ambao tumeingia mkataba na kampuni binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mkakati wetu tulikusudia kwamba tuweze kutumia utaratibu wa nukta, kwamba mtu atakapokuwa amefanya makosa aweze kupunguziwa points na baadaye ikiwezekana leseni yake ipunguzwe. Mkakati huu umeshindwa kufanikiwa kwa sababu ya utaratibu wa huu mfumo tulionao. Tunatarajia baada ya mkataba huu kumalizika Juni tutaingia katika mfumo ambao umeandaliwa na Jeshi la Polisi, mfumo huu tunatarajia kuoanisha na mfumo unaotumika TRA ili tuweze sasa kutumia utaratibu wa nukta na hii itasaidia sana kuweza kupunguza ajali za barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto ya matumizi ya teknolojia ambayo Waheshimiwa Wabunge wamezungumza. Hili ni jambo ambalo katika mkakati wetu wa awamu ya pili tunatarajia kuanzisha na tutalipa kipaumbele ikiwemo utaratibu wa kuweza kuweka vidhibiti mwendo badala ya kutumia hizi tochi za sasa hivi ambazo zinatumika barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kuna mambo mengine ambayo yamezungumzwa kuhusiana na changamoto za Askari wetu wa barabarani. Nataka tu nichukue fursa hii kutoa takwimu za haraka kwamba kuna Askari wengi sana ambao katika kipindi cha mkakati huu katika mambo 14 tuliyoyazungumza kwamba tutahakikisha tunashughulikia wale ambao wanakiuka maadili wakati huo huo tunawapongeza wale ambao wanafanya vizuri. Kuna orodha ndefu ya Askari ambao wamefanya kazi vizuri na kuna orodha ndefu yaAskari ambao tumewapongeza ambapo mara nyingi hawa ambao wanafanya kazi nzuri ambao ndiyo wengi huwa hawaonekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni kwamba tunatarajia kuanzisha awamu ya pili ya mkakati wetu wa kupunguza ajali, baada ya kuona mafanikio na upungufu ambao nimeuzungumza, sasa hivi tunajikita zaidi katika kuangalia utaratibu wa aina ya madereva waliopo nchini mwetu. Leo hii naomba nichukue fursa hii kukazia maagizo ya Mheshimiwa Makamu ya Rais aliyoyatoa juzi kuhusiana na kuhakikisha kwamba ukaguzi wa kina unafanyika kwa upande wa madereva ya mabasi ya wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichukue fursa hii kutoa maagizo hapa kwa Jeshi la Polisi kuanza operesheni maalum ya kusaka na kukagua mabasi ya wanafunzi pamoja na madereva ambao wanaendesha magari haya ili sasa hivi tuweze kuona kwamba eneo hili ambalo lilisahaulika kwa kiasi fulani, liweze kupewa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia hali ya usalama barabarani, naomba sasa niingie katika hali ya kisiasa kwa ujumla wake. Upande wa hali ya kisiasa nchi yetu ipo salama juu ya matukio na changamoto za hapa na pale, hali ya usalama kwa ujumla katika nchi yetu ni ya kuridhisha. Tumepita katika kipindi kigumu sana, katika kipindi cha mwaka mmoja nchi yetu imekumbana na majaribu mbalimbali na ninyi ni mashahidi. Tumeweza kuona matukio ya uhalifu ya aina yake ambayo yametokea kule katika Mikoa ya Mwanza, Tanga, maeneo ya Mbagala na mengine ambayo yamehusisha mpaka uuaji wa Askari wetu. Yote haya ambayo yamejitokeza katika kipindi cha nyuma tuliahidi hapa Bungeni kwamba tutashughulika nayo na tumeshughulika nayo kwa mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ambayo inaendelea kujitokeza sasa hivi katika Mkoa wa Pwani, nina hakika tutafanikiwa kuweza kudhibiti hali ile na hali ya usalama iweze kurudi kama kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kusisitiza vilevile jambo lingine la muhimu sana na la msingi kwamba katika kufanikisha lengo hili ni lazima wananchi watoe mchango mkubwa, wananchi ndiyo ambao wanakaa na jamii na wahalifu huko. Kwa hiyo, bila kulisaidia Jeshi la Polisi kazi hii inaweza isiwe na ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya usalama Zanzibar; Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia jambo hili, kimsingi ni kwamba hali ya usalama Zanzibar nayo ni shwari. Nilisikitika sana nilipofanya ziara kama ambavyo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge nilipotembelea Majimbo yao akiwemo Mheshimiwa Mwantakaje kuona kwamba katika Zanzibar ambayo naifahamu mimi kuna baadhi ya maeneo yalikuwa hawezi kupita raia. Nachukua fursa hii kulipongeza sana Jeshi la Polisi kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya kuweza kuhakikisha maeneo yale yanaendelea kurudi katika hali ya kawaida na wananchi wanafanya kazi zao kwa usalama na amani. Kwa hiyo, hali ya usalama kwa ujumla katika nchi yetu inaendelea kuimarika na itazidi kuimarika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine ambalo limezungumzwa; suala hili la mgogoro wa Chama cha CUF. Hapa hatuwezi kupoteza muda kuzungumza migogoro ya Vyama vya Siasa, hiyo siyo kazi yetu. Jeshi la Polisi linafanya kazi yake kwa mujibu wa sheria, weledi na maadili. Kama kuna vyama ambavyo labda maji yapo shingoni migogoro yao imewashinda wenyewe kwa wenyewe wanatafuta mtu wa kumsuluhisha, siyo kazi ya Jeshi la Polisi. Jeshi la Polisi kazi yake ni kusimamia sheria, ndiyo maana nasema kwamba matukio ambayo yametokea ya ugomvi wa vyama vya siasa wenyewe kwa wenyewe hatuwezi tukaruhusu umwagaji wa damu wa raia yeyote. Kama mna migogoro yenu, mtafute njia sahihi ya kuirekebisha. Anapotokea mfuasi wa chama chochote, iwe ndani ya chama hicho hicho anawasilisha taarifa kwa Jeshi la Polisi juu ya mwelekeo wa uvunjifu wa amani, Jeshi la Polisi haliwezi kuruhusu hiyo hali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inashangaza sana, kwamba leo asubuhi nimeangalia TV Channel Ten, nimeona kwenye taarifa ya habari ya Channel Ten leo hivi asubuhi kwamba Chama cha CUF, wamefanya mkutano wa hadhara uliovyoelezwa na Waandishi wa Habari kwa mujibu wa TV ya Channel Ten, wamefanya mkutano wa hadhara na mazingira yameonesha ni mazingira ya maandamano. Nataka nimuagize IGP hapahapa kulichunguza hilo jambo. Tumepiga marufuku mikutano ya hadhara isipokuwa kwa Wabunge wa Majimbo hayo, tumeona watu wamekusanyika wameenda kufanya mikutano ya hadhara, hilo jambo lazima lichunguzwe na hatua stahiki zichukuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sipo hapa kujibu hoja za Mheshimiwa Khatib maana marehemu Bibi yangu alinifundisha hadithi moja kwamba kama umeenda kuogelea baharini halafu akatokea mwendawazimu akachukua nguo zako huwezi kumkimbiza, wewe utaonekana mwendawazimu zaidi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la Magereza. Katika jambo ambalo ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais ambalo ni aibu kwamba kwa idadi ya nguvukazi ya wafungwa tulionao na kwa idadi ya rasilimali ya mashamba makubwa tuliyonayo katika maeneo ya Magereza haiwezekani hata siku moja, hatuwezi kukubali chini ya uongozi wa Wizara hii ikiwa Mheshimiwa Mwigulu ni Waziri na mimi Naibu Wake namsaidia, kuona kwamba jambo la Wafungwa kuendelea kula bure, hali ya kuwa tuna mashamba yenye nafasi ya kutosha na tuna rasilimali na nguvukazi ya kutosha. Tumejipanga vizuri katika hilo kuhakikisha kwamba utegemezi wa chakula katika Magereza yetu unapungua kama siyo kwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya idadi ya Magereza yetu ni 129 ambayo yana jumla ya ekari zaidi ya 300,000. Miongoni mwa Magereza haya, ya kilimo ni 48 ambayo yana takribani ekari zaidi ya 150,000. Kuna mikakati kadhaa ambayo tumeichukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja; tumejaribu kuangalia uwezekano wa kuwavutia Wawekezaji waweze kushirikiana na Jeshi la Magereza kuzalisha. Nichukue fursa hii kuyapongeza sana mashirika yetu ya pensheni, leo tunapozungumza hapa Gereza la Mbigiri tayari wameshaingia mkataba na NSSF katika kuzalisha siyo tu miwa vilevile kuanzisha kiwanda cha sukari. Wakati jitihada hizo za kuvutia wawekezaji werevu zikiendelea, tunaendelea kuhakikisha kwamba Magereza ambazo zipo karibu na mito tunaanzisha kilimo cha umwagiliaji kama ambavyo tumefanya katika baadhi ya Magereza mfano, Idete, Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi tuna mpango katika kipindi chetu hiki cha mwaka mmoja unaokuja kuhakikisha kwamba tume-earmark Magereza 11 kwa ajili ya kuzalisha pamoja na mifugo katika kilimo cha mpunga, mahindi na mawese. Matarajio yetu ni kwamba tuzalishe takribani tani 13,260 kwa kutumia Magereza hayo ambayo tumeyachagua. Mahitaji ya sasa hivi ya chakula kwa wafungwa ni takribani tani 10,740, tutakapozalisha tani 13,260 tuna uwezo wa ku-cover mahitaji yote ya wafungwa, wakati huo tukaweza kuwa na chakula cha ziada cha takribani tani 2,500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kutusaidia kupata matrekta 50 ambayo mchakato wake umeshaanza, kati ya hayo matrekta 50 yatakayopatikana yatasaidia kuhakikisha kwamba mpango wetu huu wa kuhakikisha kwamba Magereza yanajitegemea kwa kilimo unafanikiwa, leo hii matrekta matatu tayari yapo katika Gereza la Mbigiri kwa ajili ya shughuli za kilimo cha miwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na maagizo ya Mheshimiwa Rais kwamba wafungwa wafanye kazi, tumehakikisha kwamba tumefanya kazi hiyo na mafanikio yake ni makubwa sana. Siyo tu kwamba wafungwa hawa watashirikishwa katika kilimo, leo hii Mheshimiwa Rais ametoa shilingi bilioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Magereza Ukonga, leo hii nimesimama hapa nikiwa nimefarijika sana, kwamba tumefanikiwa kuokoa takribani nyumba 80 za ziada kwa kuwatumia wafungwa, jambo ambalo pengine tungetumia utaratibu mwingine nyumba hizi 80 tusingeweza kuzipata kwa ajili ya nyongeza ya Askari wetu. Kwa hiyo, hiyo ndiyo faida ya kutekeleza maagizo ya Mheshimiwa Rais ya kuhakikisha kwamba wafungwa tunawatumia ipasavyo siyo tu kwa kuzalisha lakini kwa kusaidia kuwajengea uwezo ili waweze kwenda kujitegemea watakapotoka huko kwenye Magereza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kana kwamba hiyo haitoshi, tayari tuna programu mbalimbali za kurekebisha wafungwa katika Magereza yetu mbalimbali ambayo sina haja ya kuyataja kutokana na muda kwani yapo mengi. Katika bajeti yetu ya mwaka huu tumewekeza takribani shilingi bilioni 2.2

ambazo zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kuimarisha viwanda vidogovidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia ushiriki wa Magereza katika uchumi wa viwanda hatuzungumzii viwanda vikubwa tu, mpaka viwanda vidogovidogo, tunapozungumzia viwanda vya karanga Mbigiri, lakini wenyewe ndani ya Magereza kuna viwanda kwa mfano, katika bajeti hii katika fedha hizi tunatarajia kuanzisha kiwanda cha helmet pale Ukonga, kiwanda cha useremala Isanga, Dodoma, kwenye kambi ya Kimbiji tunatarajia kununua mashine vilevile kwa ajili ya kiwanda cha kuzalisha mawese, pamoja na Gereza la Lindi - Machole ambapo kuna kiwanda cha chumvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na muda, naomba niende kwenye Jeshi la Zimamoto. Jeshi la Zimamoto jambo kubwa na la msingi ambalo tunaliwekea kipaumbele ni kuhakikisha kwamba tunapata kwanza vifaa vya kutosha ili tuweze kudhibiti majanga ya moto yanapotokea, pia vifaa hivi viweze kuenea katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu hasa katika Wilaya ambapo huduma hii haijafika. Hivi sasa kuna huduma ya Zimamoto katika mikoa yote lakini kuna wilaya nyingi ambazo bado huduma hii haijafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii katika kipindi cha mwaka mmoja tunajivunia mafanikio makubwa kwamba, tumeweza kuanzisha Zimamoto katika Ofisi za Wilaya takribani nne ikiwemo Ruangwa, Ukerewe, Ileje na Rungwe. Nilipokwenda Ruangwa na Rungwe tuliwaahidi kwamba tutawapatia gari. Bahati mbaya zile gari tulizoahidi zimepata changamoto lakini hii ahadi iko palepale, gari nyingine zitakapofika kipaumbele kitaelekea katika maeneo ambayo tumetoa ahadi ili yaweze kusogeza nguvu na jitihada ambazo tayari zimeoneshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi wakati mkakati huu wa kueneza huduma ya Zimamoto Wilayani unaendelea, tunaanza kupeleka huduma ya elimu katika wilaya zetu, kuhakikisha kwamba tunatafuta Askari kwa ajili ya kupeleka elimu ya kinga na tahadhari ya moto. Hilo jambo limekuwa likifanyika kwa mafanikio makubwa katika maeneo mbalimbali nchini na tunaomba Waheshimiwa Wabunge watuunge mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba katika bajeti hii tumetenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa magari manne, kuna mkakati kabambe utakapofanikiwa wa kupata mkopo wa fedha zitakazosaidia kupata vifaa vya kisasa kupitia mkopo wa Benki ya KBC chini ya kampuni ya Smart ambayo mazungumzo yanaendelea vizuri. Tunatarajia katika mpango huu kununua magari 21 pamoja na vituo vitatu vya kisasa vya zimamoto na uokoaji katika Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunatarajia kuingia mkopo mwingine waEuro milioni tano ambapo unatarajia kutolewa na Serikali ya Austria kupitia Raiffeisen Bank ambapo tunatarajia kununua magari pamoja na vitendea kazi vingine. Kwa hiyo, utaona kwamba kuna jitihada kubwa ambazo tumezichukua katika kuhakikisha kwamba tunaimarisha vitendea kazi katika Jeshi la Zimamoto pamoja na kuweza kusogeza huduma hizi karibu na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie Mamlaka ya Vitambulisho (NIDA). Kabla sijazungumzia Mamlaka ya Vitambulisho (NIDA), kabla kengele yangu haijalia, naomba nichukue fursa hii kuwatambua kwa haraka, maana niwatendee haki Waheshimiwa Wabunge wametoa michango mizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumzia hoja ya usalama barabarani ambayo Mheshimiwa Lucy Owenya, Mheshimiwa Mbaraka Dau, Mheshimiwa Balozi Adadi Rajab, Mheshimiwa Maulid Mtulia, Mheshimiwa Dkt. Immaculate Semesi, Mheshimiwa Leah Komanya, Mheshimiwa Mwita Waitara, Mheshimiwa Oscar R. Mukasa, Mheshimiwa Raza, Mheshimiwa Risala Kabongo, Mheshimiwa Zainab Mussa Bakar, hawa walichangia wengine kwa maandishi na wengine kwa kuzungumza hii hoja ya usalama barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa hoja ya hali ya kisiasa, Mheshimiwa Katani Katani, Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mheshimiwa Makilagi, Mheshimiwa Bobali, Mheshimiwa Faida, Mheshimiwa Khalifa Mohamed Issa, Mheshimiwa Maftaha, Mheshimiwa Sofia Mwakagenda, Mheshimiwa Mnyika, Mheshimiwa Mtolea, Mheshimiwa Rhoda Kunchela na Mheshimiwa Mwantakaje pamoja na Mheshimiwa Ali King walichangia kwa kiasi fulani kwa maandishi na kwa kuzungumza hoja ya hali ya kisiasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya Magereza wachangiaji walikuwa ni wengi vilevile; Mheshimiwa Japhet Hasunga, Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mheshimiwa Risala Kabongo, Mheshimiwa Esther Matiko, Mheshimiwa Gekul, Mheshimiwa Mkuchika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika hii hoja ambayo nimemaliza nayo muda huu mfupi uliopita ya zimamoto; Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mheshimiwa Japhet Hasunga, Mheshimiwa Maftaha Nachuma, Mheshimiwa Juliana Shonza, Mheshimiwa Shaabani Shekilindi, wote hawa walichangia hii hoja ya zimamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa hii hoja ambayo namalizia sasa hivi ya NIDA, kuna wachangiaji wawili ambao walichangia kwa maandishi, Mheshimiwa Magdalena Sakaya na Mheshimiwa Bobali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwatambua Waheshimiwa Wabunge kutokana na michango yao mizuri, naomba sasa nimalizie kwa haraka hoja ya Mamlaka ya Vitambulisho (NIDA). Kuna hoja mbili kubwa ambazo zilizungumzwa. Moja, ni kwamba malengo hayajafikiwa, tulikuwa tuna target ya kufikia malengo ya kusajili watu zaidi ya milioni 22, mpaka mwezi wa Machi tumesajili zaidi ya watu milioni nane, wakasema kwamba inakuwaje hali hii inajitokeza wakati tayari tumeshapata BVR kutoka Tume ya Uchaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba BVR za Tume ya Uchaguzi zina changamoto zake. Kwanza BVR za Tume ya Uchaguzi zinatambua taarifa zisizozidi 40 wakati taarifa ambazo zinahitajika kutumika na mfumo wa NIDA ni taarifa 72, hilo moja. Hata quality ya picha nafingerprints kwa upande wa mfumo huu wa BVR…

(Hapa muda kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuwa na imani nami kwa nafasi hii ya Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii vilevile kumshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kwa miongozo ambayo wanaendelea kutupatia katika kutekeleza majukumu yetu ya kila siku.

Namshukuru vilevile Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba pamoja na Watendaji, Makamanda na Maofisa wote waliopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi nikianzia na Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Wakuu wa Vikosi na Taasisi mbalimbali kwa ushirikiano wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, naishukuru sana familia yangu kwa ujumla pamoja na wananchi wa Jimbo langu la Kikwajuni kwa kuendelea kuniunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nianze moja kwa moja kuchangia mada ama maoni mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge ambayo yaliwasilishwa kwa njia ya maandishi na kwa njia ya kuzungumza. Ili kuokoa muda, naomba niwatambue Waheshimiwa hawa Wabunge ambao wamechangia baada ya kutoa ufafanuzi wa hizi hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa pamoja natarajia kuzungumzia mambo kama manne kama muda utaruhusu. Kwanza kabisa naomba nizungumzie suala la usalama barabarani. Hii ni moja katika hoja ambazo zimeibuka kwa kiwango kikubwa sana kwa Waheshimiwa Wabunge. Nachukua fursa hii kuwapongeza sana Waheshimiwa Wabunge kwa jinsi ambavyo wanaonekana wanaunga mkono jitihada za Serikali za kupunguza ajali nchini ambazo zimekuwa zikipoteza maisha ya Watanzania wenzetu na wengine kuwaacha vilema kwa miaka mingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inadhihirisha sasa hivi katika Bunge letu Tukufu kuna Chama cha Mabalozi wa Usalama Barabarani chini ya Mwenyekiti Mheshimiwa Adadi. Nawapongeza sana kwa jitihada hizo. Kuungwa mkono kwao, kwetu sisi Waheshimiwa Wabunge kumechangia leo hii kusimama mbele yenu tukijivunia mafanikio makubwa sana ambayo tumefikia kwa kupunguza ajali hizi chini kwa wastani wa asilimia 35.7 toka mwezi Julai, 2017 mpaka Machi mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi ni mashahidi, katika miaka ya nyuma hapa tulikuwa tunashuhudia ajali nyingi zimetokea hasa mwisho wa mwaka, watu wengi walikuwa wanafariki lakini sasa hali hiyo imepungua kwa kiwango kikubwa. Mafanikio hayo yametokana na kazi kubwa ambayo tunaifanya kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Baraza la Usalama Barabarani na Kikosi cha Usalama Barabarani cha Jeshi la Polisi tuliandaa mikakati kabambe ya kupunguza ajali hizo ambapo leo hii tunazungumzia utekelezaji wa mkakati wa awamu ya tatu, tunaenda nao. Katika kila mkakati, tunaangalia upungufu wa mkakati wa kwanza kurekebisha tunapoingia katika mkakati unafuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kwamba maoni yaliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge leo hapa yatasaidia sana katika kurekebisha upungufu uliojikoteza ili mkakati wetu wa awamu ya tatu tunaoenda nao uweze kuwa na mafanikio zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla hatujazungumza suala la ajali barabarani lazima tujue vyanzo vya ajali barabarani ni nini? Vyanzo vikubwa vya ajali barabarani ni vitatu. Cha kwanza ni upungufu wa kibinadamu ambao mara nyingi unatokana na uzembe na hiki ndio chanzo ambacho kinachangia kwa wastani wa asilimia 76 na vyanzo vingine viwili ikiwemo ubovu wa magari na ubovu wa miundombinu vinafuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia chanzo cha binadamu maana yake mikakati yake ni lazima ilenge katika kushughulikia na changamoto ambazo wanadamu hawa wanasababisha ajali. Ukifanya hivyo maana yake utawagusa hawa binadamu ambao ni wananchi na raia wa nchi hii ambao sisi Waheshimiwa Wabunge ndio tunawawakilisha katika Bunge hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamezungumzwa hapa, kwa mfano wapo Waheshimiwa Wabunge waliosema kwamba Askari wetu wa Usalama Barabarani hawana muda wa kutoa elimu, wamekuwa wakitoa fine kwenda mbele tu. Wako ambao walizungumzia kuhusiana na utaratibu mzima wa namna ya utoaji fine, hawajaridhika nao. Yote haya yanalenga katika madereva ambao hao binadamu wanasababisha matatizo ya ajali kwa makosa ya kibinadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mifano miwili, mitatu kuthibitisha hili. Nikichukua ajali za mwisho kubwa zilizotokea, maana bahati mbaya sana ajali za barabarani zikitokea zinavuta hisia nyingi sana kwa jamii kiasi kwamba yale mafanikio makubwa ambayo tunayazungumzia yanafichika. Ikitokea ajali moja inaweza ikaua watu hata 20 kwa mpigo na Taifa linapata taharuki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mifano miwili ya karibuni hii ya mwisho. Kuna ajali ambayo ilitokea tarehe 9 Aprili, kule Mbeya ambapo Lori la Scania lilihama njia na kuifuata Noah. Hao wananchi wasiokuwa na hatia waliokuwa kwenye Noah walikuwa wanaelekea msibani takriban familia nzima. Basi lile likaenda kuivaa ile Noah na kuua takriban watu wanane na kusababisha majeruhi mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchunguzi tulioufanya, chanzo cha ajali hii ni kwamba basi hili liliacha njia na dereva yule sijui alikuwa amelewa au amelala, lakini aliifuata Noah ile na kusababisha ajali ya watu wengi hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajali nyingine ambayo ilitokea tarehe 24 mwezi wa Tatu maeneo ya Mkuranga, Lori la Scania vilevile liliacha njia na kuivaa Hiace. Katika ajali hii walikufa watu 24 na majeruhi takriban 10. Tatizo lilikuwa ni mwendokasi. Hizo hizo changamoto za kibinadamu tunazozizungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika hali kama hii na uzembe huu ambao unasababishwa na baadhi ya madereva, mbali na jitihada kubwa za utoaji elimu ambao tunafanya, leo hii mkifungua vipindi vya redio na TV mtakuta Askari wetu wakitoa elimu kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna utaratibu wa kutoa elimu kwa jamii na makundi mbalimbali, utaratibu hata wa kutoa elimu kabla dereva hajapata leseni ndio aingie barabarani. Juu ya jitihada hizi bado kuna changamoto za madereva ambao wamekuwa hawafuati sheria za barabarani na wamesababisha vifo vya watu wengi wasiokuwa na hatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hali kama hiyo, elimu ambayo inabakia, elimu hiyo itatolewe katika Gereza. Maana Gerezani moja ya kazi yake ni kurekebisha tabia za watu waliofungwa, lakini hata kufungiwa leseni na ndiyo maana sasa hivi tunaelekea katika mpango wa kuanzisha utaratibu wa nukta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakapofanikiwa kuoanisha mifumo yetu hii wa Polisi na TRA tuweze sasa kufungia leseni mifumo hii ikisomana, lakini itakwenda sambamba na malengo yetu kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amezungumza katika hotuba kwamba sasa suala la leseni tunataka libakie katika Polisi ili kuepusha urasimu usiokuwa na faida. Lingine ni elimu kwa utaratibu wa kutoa fine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge tunaomba sana mwendelee kuunga mkono Serikali yenu inapopambana kuhakikisha kwamba inaokoa uhai wa wananchi wanaokufa na wengine kupata vilema bila hatia. Vile vile tunaendelea kutoa elimu. Kwa sauti hizi za Wabunge hatuwezi tukazidharau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kusema ni kwamba, nitoe wito kwa baadhi ya Maafisa wetu wa Traffic ambao wanatumia fursa hii vibaya, wachache, kama wapo kuacha tabia hii. Maana makosa mengine ni madogo madogo. Unaweza kukuta mtu pengine kwenye foleni kubwa katika Jiji la Dar es Salaam, halafu hajafunga mkanda unamtoza faini badala ya kumwelekeza. Mambo kama hayo, nadhani wanatusikia, waweze kuzingatia. Tunazungumzia yale makosa hatarishi, lakini yapo makosa madogo madogo ambayo tunadhani wanaweza wakaanza kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine hatutaki baadhi ya Maafisa wetu wa Serikali ama wa vyombo hivi waitie madoa Serikali yetu. Waendelee kusimamia sheria lakini waendelee vilevile kuangalia mazingira na uzito wa makosa yenyewe kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lilikuwepo suala la masuala ya notification. Wapo Waheshimiwa Wabunge walilalamika wakasema kwamba kuna wakati mwingine wanapewa notification lakini hawapewi risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu kwa ufupi. Ni kwamba bahati mbaya sana hizi mashine tulikuwa nazo katika Mikoa miwili ya Dar es Salaam na Pwani, lakini nataka nichukue fursa hii kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge kwamba tayari tumeshapata mashine takriban 3,000, tunatarajia kuzisambaza mikoani kwa awamu. Zitakapokamilika kutawanywa kote, ambapo sasa hivi tunaanza Arusha na mikoa mingine saba ambayo imeanza kupewa elimu, nadhani changamoto hii itaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wasiwe na hofu, notification ile ina kumbukumbu zote, hakuna mwananchi ambaye atapewa notification, halafu fedha ile isiende kwenye mamlaka husika na iingie mfukoni kwa mtu binafsi. Kwa hilo, tumejiridhisha kwamba kwa mfumo uliopo vilevile fedha hizi ziko salama. Hata hivyo jambo hili tunatarajia kulikamilisha hivi karibuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niingie katika eneo la pili. Jambo la pili ambalo nataka nilichangie ambalo nimekuwa nikilijibu kwa muda mrefu sana katika Bunge letu hili Tukufu ni kutokana na Waheshimiwa Wabunge wengi wa Bunge hili kuguswa na hali ya mazingira ambayo askari wetu wanafanyia kazi. Kama tunavyojua, askari wetu hawa wanafanya kazi ngumu sana katika mazingira magumu. Moja katika mazingira magumu ambayo wanafanyia kazi ni maeneo ambayo wanaishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Waheshimiwa Wabunge leo tukitoka hapa Bungeni baada ya kazi ngumu ya kuwawakilisha wananchi, halafu turudi nyumbani mazingira yakiwa siyo mazuri, nadhani hata concentration ya kazi siku ya pili haiwezi kuwa nzuri. Askari wetu wamekuwa wakifanya kazi hii kwa mafanikio makubwa kwa miaka yote na ndiyo maana nchi yetu iko salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi cha miaka ya mwanzo hapa wakati tunaingia, suala hili nilikuwa nikilijibu na nilikuwa nikisema, jamani tuna mpango wa kujenga nyumba 4,136 kupitia mkopo wa Exim Bank. Baadaye Waheshimiwa Wabunge wengine katika michango yao wakadiriki kusema kwamba tunawapiga danadana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie tu kwamba wakati mwingine danadana nyingine zinakuwa ni kwa maslahi yetu sisi wenyewe na maslahi ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nachukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais. Nadhani sasa hivi wananchi takriban wote wa Tanzania wameshamfahamu, labda wale wasiotaka tu kwa sababu ya ajenda zisizokuwa za msingi. Mheshimiwa Rais wetu amekuwa mara zote akipigania matumizi sahihi ya rasilimali zetu, kwamba fedha ambazo zinatoka za wananchi zitumike kwa ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni mfano mmojawapo. Kwamba mradi huu ambao tulikuwa tunatarajia kupata mkopo wa takriban shilingi bilioni 500 kupitia Exim Bank ambao ungejenga nyumba kama 4,136 ukiachia gharama nyingine za Bima, Consultation Fee na kadhalika, unakuta ungeweza kugharimu wastani wa kama dola milioni mia nne na kitu ambapo kwa hesabu ya harakaharaka ukigawa kwa nyumba 4,136 unaweza ukapata dola takriban 98,000, unazungumzia shilingi milioni 220 mpaka 240, nyumba moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais juzi ametoa shilingi bilioni 10 baada ya kujiridhisha juu ya ujenzi wa nyumba ambazo tunajenga kwa kutumia rasilimali zetu za ndani kwa nyumba moja ya Polisi kugharimu shilingi milioni 25. Unaona tofauti hiyo kubwa! Takriban mara kumi au mara tisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungekubali kwenda haraka na mradi ule ambao tumeukuta, tungeweza kupoteza fedha za wananchi ambazo zingeweza kutumika kwa kazi nyingine, lakini tungeweza vilevile kupata nyumba za ziada kwa askari wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge wafahamu kwamba Serikali yenu ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, ni Serikali makini na inayotoa maamuzi yake kwa maslahi ya Taifa na wananchi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunazungumzia hatua ambayo tunakwenda nayo katika kupunguza changamoto ya ujenzi wa nyumba za Askari wa aina zote tukianzia Magereza, Polisi, Uhamiaji na kwingineko, mpaka Fire na kwingine tutafika huko. Nataka nitoe mfano mmoja. Katika mradi wa Arusha ambapo Mheshimiwa Rais aliuzindua juzi, tulijenga takriban nyumba 31.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais baada ya kuungua zile nyumba alitoa shilingi milioni 250. Nachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Comrade Gambo kwa kuhamasisha wadau mbalimbali tukaweza kujikuta tunatumia fedha hizo kujenga nyumba 31. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano huo huo, tumefanya Pemba. Kuna ujenzi wa nyumba unaendelea Pemba tunavyozungumza sasa hivi. Nachukua fursa hii kuwapongeza Wakuu wa Mikoa wote wawili; wa Mkoa wa Kaskazini na Mkoa wa Kusini na wadau mbalimbali walioshiriki. Kuna programu ya ujenzi wa nyumba 36 Pemba. 12 Unguja, 24 Pemba na tayari nyumba 12 tunatarajia zitakamilika kabla ya kumalizika kwa mwaka huu kwa sababu vifaa vyote vya ujenzi wa nyumba zile vipo, vimepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naendelea kutoa wito na kusisitiza Jeshi la Polisi kuzingatia maagizo ya Mheshimiwa Rais pamoja na Wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa kutumia fedha hizi zilizotolewa, shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Polisi zitumike kama zilivyokusudiwa. Wahamasishe wadau katika mikoa yao ili tuweze kupata nyumba nyingi zaidi. Lengo letu ni tunatarajia katika pesa hizi tutapata nyumba takriban 400 kwa kuanzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vipaumbe vyetu kwanza ni Mkoa wa Dodoma ambapo ni Makao Makuu ya Serikali, yameshahamia. Maeneo mengine ni mikoa yote mipya ya Kipolisi; Simiyu, Njombe, Katavi, Geita, Songwe, Rufiji, Pwani pamoja na Zanzibar. Haina maana kwamba tutaacha maeneo mengine. Ninachozungumza ni kwamba mgawanyo unaangalia ukubwa wa changamoto katika maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kwamba kwa utaratibu huu wa kutumia rasilimali zetu vizuri na leo hii tunazungumzia kuimarisha kikosi chetu cha ujenzi katika Jeshi la Polisi (Police Building Brigade) ambayo tumeiwezesha kwa kuongeza idadi ya wafanyakazi na kuwapatia mafunzo mbalimbali, hali kadhalika kwa upande wa Magereza, tunafanya hivyo hivyo. Ndiyo maana nyumba ambazo tunajenga Ukonga kwa fedha ambazo Mheshimiwa Rais ametoa kwa utaratibu huo huo, takriban 320, mchango wa Kikosi cha Ujenzi cha Jeshi la Magereza, wafungwa na rasilimali zilizopo kwa kweli unafanikisha sana kufanya tujenge kwa fedha hizi kwa unafuu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uhamiaji ni mashahidi, juzi Mheshimiwa Rais amezindua nyumba 103 pale Dodoma. Kwa hiyo, tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini katika miaka michache inayokuja, masuala yenu kuhusiana na changamoto ya makazi kwa askari wetu itakuwa inapungua, haitakuwa tena ni swali la kila siku katika Bunge hili kwa kasi hii. Kwa hiyo, hayo ni moja ya maelezo yangu katika eneo la nyumba za Askari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nizungumzie kwa haraka haraka suala la Uhamiaji haramu. Kwanza nataka nirudishe kumbukumbu nyuma. Wakati Serikali hii inaingia madarakani, tulikuwa tuna tatizo kubwa la wahamiaji haramu katika nchi hii. Mtakumbuka miaka miwili iliyopita tulifanya operesheni kabambe na tukafanikiwa kuwaondoa wengi sana katika mikoa yote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa operesheni hiyo kwa kushirikiana na Wizara yenye mamlaka ya Kazi chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tuliweza kukagua makampuni 429 na watuhumiwa takriban 2,199 walikamatwa kwa makosa mbalimbali ya Uhamiaji. Hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kufikishwa Mahakamani, wengine waliondolewa nchini, wengine walihalalishwa ukazi wao na vilevile tukafanikiwa kuweza kukusanya maduhuli ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumetengeneza nidhamu katika nchi yetu kwamba sasa nchi yetu siyo sehemu ambayo unaweza ukaja tu ukaishi kiholela bila kufuata utaratibu; kwamba unaweza ukaja hapa ukafanya kazi ambazo Watanzania wanaweza kuzifanya, kwamba unaweza ukaja hapa ukajifanya ndio una nguvu zaidi ya kunyanyasa wananchi wa nchi hii. Kuna vijana wetu ambao wangeweza kutumia fursa hizi wakatumia watu wengine wa nje ya nchi bila sababu ya msingi. Nidhamu hiyo imerudi katika nchi yetu kwa kazi kubwa ambayo tumeifanya na tunaendelea kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, operesheni hizi zilikuwa zimetengeneza misingi, maana nchi yetu haiwezi kuendeshwa kwa operesheni. Tumeleta operesheni kutengeneza misingi na mifumo ambayo sasa hivi tunaendelea nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka mmoja huu uliopita, tunazungumzia wahamiaji haramu takriban 13,000 waliokamatwa na kuchukuliwa hatua mbalimbali na wengine kushtakiwa, lakini idadi hii kubwa inahusisha pia wale wapitaji haramu. Nataka niseme kwamba wote ni wahamiaji haramu lakini najaribu kutofautisha ili nieleweke vizuri na hasa wale raia wa Ethiopia. Wako Waheshimiwa Wabunge ambao walisema kwa nini tusiwarudishe kwao? Kwa nini tusiwasindikize tu wakaenda wanapoenda midhali hawakai hapa nchini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivyo siyo tu kukiuka Sheria za Uhamiaji, lakini vilevile ni kukiuka Sheria za Kimataifa kuhusiana na biashara haramu ya kusafirisha binadamu. Kwa hiyo, kama nchi yetu ambayo tunaheshimu misingi ya utawala bora, hatuwezi kufanya hivyo. Tunachokifanya ni kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha kwamba jambo hili linakoma na ni endelevu, badala ya kukimbizana nao kila siku, ili rasilimali zetu chache tulizonazo katika vyombo hivi likiwemo Jeshi la Uhamiaji, ziweze kutumika kwa mambo ambayo yana faida zaidi, sisemi kwamba hili halina faida, lakini tuna changamoto nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mkakati kabambe ambao tumeuandaa wa kudhibiti mipaka yetu ambao utahitaji fedha nyingi sana ikihusisha ujenzi wa Mobile Immigrations Posts katika mipaka yetu na kwenye vipenyo vyote tulivyovihesabu katika nchi hii. Kwa kuanzia tunaweza kuanza na vipenyo takriban 107 ambavyo ni vipenyo sugu pamoja na vifaa vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati hayo yanaendelea, tunaomba ushirikiano kwa wananchi katika kupambana na tatizo hili, maana wahamiaji haramu hawa wengine tunaishi nao, wengine wanatoa majumba yao kuwahifadhi hawa. Moja katika mikakati yetu, tunasema kwamba tunataka tufumue mtandao wote wa wasafirishaji wa biashara hii haramu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri katika hilo tumeshaanza kufanikiwa. Japo najua jambo hili halitachukua muda mfupi, lakini tayari tumekamata watuhumiwa kadhaa ambao miongoni mwao wanahusika na bishara hizi kwamba ni wenyeji, wengine ni wananchi wa nchi hii, maana haiwezi kuwa mtu ambaye anatoka nchi nyingine akafahamu mazingira ya nchi yetu ya kupitisha hawa watu. Kwa hiyo,


wapo watu ambao tayari tumeshawashikilia na sheria inafuata mkondo wake. Katika hili naomba sana wananchi ushirikiano na msaada wenu kulifanikisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kuna mikoa ambayo ina changamoto nyingi, hasa Mkoa wa Kigoma. Wapo Wabunge wa Kigoma walizungumza hapa kwa masikitiko na wengine wameandika. Nataka niwakumbushe tu kwamba hata takwimu zetu zinaonesha kwa mazingira ya jiografia ya Kigoma ambayo inapakana na nchi jirani zetu tatu, Mheshimiwa Nsanzugwanko ananikumbusha, ambazo zimepita katika changamoto mbalimbali za kiusalama, siyo jambo la ajabu kuona, mimi nipo zaidi kwa watu ambao wanaitwa wahamiaji haramu. Nanyi ni mashahidi, leo tuna Kambi tatu kubwa za Wakimbizi; Nyarugusu, Mtendeni na Nduta, zote zipo Mkoa wa Kigoma. Wakimbizi wengine badala ya kukaa makambini wanatoroka kuja kukaa uraiani, wengine wanaingiza silaha kutoka katika nchi zao ambazo zinatumika kufanya ujambazi hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika hali kama hiyo Serikali lazima ipeleke nguvu zaidi katika mkoa ule ili kuhakikisha usalama siyo tu wa wananchi wa Kigoma lakini wananchi wa Tanzania nzima. Ikiwa kuna upungufu katika utekelezaji wa majukumu hayo, tunayachukua na tunafuatilia. Ila lengo siyo hilo, lengo ni kuhakikisha kwamba wananchi wa Kigoma wanaendelea kuishi vizuri na kwa kufuata sheria. Tunatambua juu ya ujirani mwema uliopo katika ya mikoa yetu iliyopo mipakani yote, siyo Kigoma peke yake, lakini kuna utaratibu wa mahusiano na uingiaji na utokaji kati ya wananchi wanaotoka katika nchi moja na nchi nyingine. Utaratibu huu tutaendelea kuufuata na tunaomba wananchi wa maeneo yote waendelee kuhakikisha kwamba wanatuunga mkono katika hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kwa masikitiko makubwa, kuna baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamechangia na bahati mbaya michango yao wakaielekeza katika misingi ya dini, mingine mwelekeo wa kikabila. Sisi ni watu ambao tumepewa dhamana kubwa sana na wananchi wa nchi hii. Moja katika dhamana kubwa tuliyopewa ni kuhakikisha kwamba kauli zetu tunazozitoa katika Bunge hili zinaendelea kuhakikisha umoja na mshikamano uliodumu katika nchi yetu kwa miaka tokea nchi yetu hii imeungana na imepata uhuru na mapinduzi, unaendelea kuimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii nashangaa kwamba sisi tunakuwa ni wepesi sana kusahau juu ya matatizo mbalimbali yaliyojitokeza. Leo tunajivunia juu ya mafanikio makubwa ambayo tumefikia katika kupungua kwa uhalifu nchini. Hata ukiangalia takwimu za uhalifu, labda nitoe mfano wa nchi ambayo inaongoza kwa uhalifu duniani au Afrika; South Africa au Honduras ambayo wanasema katika watu 100,000 watu 98 wanauawa kwa njia mbalimbali, wengine wanapotea, wengine wanatekwa. Nani anajua kama pengine wakati anafanya uhalifu ule alivaa nguo yenye mwelekeo wa dini fulani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi linapofanya kazi yake katika kudhibiti uhalifu halishughuliki na dini ya mtu, halishughuliki na kabila la mtu, halishughuliki na sehemu mtu anapotoka. Wakati mwingine ni matumizi mabaya tu ya hivi vitu. Wapo watu wanatumia dini kwa manufaa ya kisiasa, kitu ambacho siyo sahihi kwa dini zote. Hakuna dini ambayo inaruhusu hilo. Wako watu kwa kukubalika tu anatumia ukanda, siyo sawa. Wapo wahalifu vilevile katika kutimiza uhalifu wao wanaweza wakatumia dini, ukanda au ukabila. Nasi hao tunawa-treat kama wahalifu wengine wowote. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge katika hili tuwe makini sana. Serikali hii ya CCM ni Serikali ya Watanzania wote ambapo Serikali hii imechaguliwa na Watanzania wa dini zote, makabila yote, maeneo yote na rangi zote na iko kwa maslahi ya watu wa aina hiyo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana leo mkimwona Mheshimiwa Rais wetu anahangaika usiku na mchana halali kwa sababu ya kuinua uchumi wa nchi hii ili faida hii ipatikane. Mkiona barabara imezinduliwa, viwanda vinajengwa, ni kwa maslahi ya watu wote wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali au Jeshi la Polisi nasi ambao tumepewa dhamana ya kusimamia, hatuwezi kukubali. Kama kuna Mbunge yeyote ana uthibitisho wa hilo basi waje watuletee, tutafuatilia. Kama kuna mtu ambaye amechukuliwa hatua kwa sababu ya misingi ya imani yake au anakotoka, Waheshimiwa Wabunge, sisi ndio wenzenu, leteni tutafuatilia na kama kuna ukweli hatua zitachukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwani kuna Maaskari wangapi ambao hili suala la usalama barabarani ambalo mmelizungumza sana mwanzo, nikiwapa takwimu za askari ambao tumewashughulikia kwa kukiuka maadili yao katika kusimamia usalama barabani mtashangaa ninyi. Kwa sababu siyo malaika! Ila haiwezekani kosa la mtu mmoja lijumuishe taswira nzima ya Jeshi la Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na kuwaomba sana wawe na imani na Serikali yao na Jeshi lao la Polisi ambalo lipo kwa ajili yao. Hawa mnaowaona, wengine wako kule, wengine hapo, wengine hawapo hapa; hawapati usingizi, hawalali ili Watanzania tulale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima tuwe fair Waheshimiwa Wabunge, kwamba wao hawaruhusiwi kuingia humu ndani wakajitetea, isiwe sababu ya sisi kuwazungumza vibaya. Hii ni nchi yetu sote, vyama hivi visitugawe wala siasa zisitugawe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisichukue muda wa Mheshimiwa Waziri wangu, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuendelea kuniamini kwa nafasi hii ya Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi. Naomba niendelee kumhakikishia kwamba nitaendelea kutokumwangusha na kuchapa kazi inavyostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nachukua fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa msaada wao mbalimbali ambao unanisadia kutekeleza majukumu yangu vizuri. Pia nachukua fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Kangi Lugola ambaye kwa kweli ni Waziri wa aina yake. Tumefanya kazi kwa ushirikiano mkubwa; pamoja na Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Wakuu wa Vyombo pamoja na Makamanda wote nchi nzima na Wakuu wa Taasisi mbalimbali wakiwemo NIDA na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia siyo kwa umuhimu, niishukuru sana familia yangu kwa kuniunga mkono na kuweza kunistahimilia pale ambapo natekeleza majukumu ya Kitaifa. Baada ya shukrani hizo, sasa nataka niende moja kwa moja kwenye hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo nataka nizungumze kwa sababu ya ufupi wa muda, nimeamua kuliweka hili mwanzo kwa sababu ni jambo nadhani ni muhimu sana. Jambo hili kwa bahati mbaya linaonekana kuleta taswira mbaya na kuichafua Serikali yetu adhimu ambayo wakati wote imekuwa ikifanya kazi kwa uadilifu, kwa ufanisi na kwa bidii kubwa na juhudi kubwa katika kuwatumikiwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuhuma hizi zisipojibiwa kwa uwazi kama ambavyo nataka nijitahidi kuzijibu hapa leo, zikiendelea kubakia kuzungumzwa kila siku zinaweza kusababisha kutengeneza chuki kati ya wananchi na Serikali yao, chuki ambazo madhara yake kwa mustakabali wa amani ya nchi yetu zinaweza zikawa kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa kuna tuhuma kwamba vyombo hasa Jeshi la Polisi na kwa maana ya Serikali kwa ujumla wake, tumekuwa tukifanya kazi zetu kwa kukandamiza baadhi ya raia kulingana na aina ya dini wanayoiamini au sehemu waliyotoka. Labda nitoe mfano mmoja hai ambao umekuwa ukizungumzwa miaka mingi, wamekuwa wakitoa mfano wa watu ambao wanawaita Mashehe wa Uamsho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikiri kwamba binafsi kwa kupata fursa ya kutumikia Serikali hii, najiridhisha pasi na shaka yoyote kwamba Serikali yetu hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na vyombo vyake ambavyo tunavisimamia wakati wote tumekuwa tukifanya kazi kwa kufuata misingi ya sheria. Kama ingelikuwa nimeshuhudia aina yoyote ya upendeleo, ubaguzi kwa misingi yoyote ile, leo ningelimwandikia barua Mheshimiwa Rais ya kujiuzulu nikakaa kule backbencher, nikawa mimi ndiyo miongoni mwa watu wa kushiriki kupingana na hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu naamini kabisa kwamba kwanza Serikali ya aina hiyo itakuwa ni Serikali ambayo inatenda dhambi kwa Mwenyezi Mungu, lakini ni Serikali ambayo itakuwa inaandaa misingi mibovu ya amani ya nchi hii. Tumeshuhudia Mataifa mbalimbali ambayo haikuwa na misingi mizuri kama misingi ambayo Waasisi wa Taifa hili waliojenga kwa Tanzania inayosababisha mpaka sasa hivi tuendelee kubakia na umoja na mshikamano bila kujali jambo lolote ambalo mhusika analo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi najua jambo hili bahati mbaya linazungumzwa na baadhi ya wanasiasa kwa sababu za kisiasa, jambo ambalo ni hatari sana, lakini hatuwezi kuendelea kukubali. Tuhuma hizi za hawa watu wa Uamsho zimekuwa za muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka katika vikao vya bajeti vilivyopita ilikuja hoja ya kwamba watu hawa wa Uamsho wanafanyiwa vitendo vya udhalilishaji na tukapata maelezo kutoka vyombo vyetu tukiwasilisha Bungeni kueleza kwamba haya ambayo yanazungumzwa siyo kweli. Nami binafsi nilifanya ziara ya kwenda Gereza la Ukonga na kuzungumza nao watu hawa. Nilipofika niliwauliza kwamba je, kuna jambo lolote la kinyume na utaratibu ikiwemo udhalilishaji ambapo vyombo vyetu vilivyopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi vimewafanyia? Wakaniambia hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilivyofika niliwauliza kwamba, je, kuna jambo lolote la kinyume na utaratibu ikiwemo udhalilishaji ambavyo vyombo vyetu vilivyopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi vimewafanyia? Wakaniambia hakuna, nikawauliza je, kuishi kwenu hapa kuna mashaka yoyote ya ukiukwaji wa haki za binadamu? Wakaniambia hakuna, tuko vizuri kabisa. Baadaye wakanieleza pamoja na mambo mengine, jambo la kwanza wakaniambia kwamba sisi changamoto yetu hapa ni kuchelewa kwa kesi yetu. Concern hiyo ndiyo concern ambayo Serikali tunayo siyo kwa wao tu bali kwa Mahabusu wote nchi nzima na kila siku tumekuwa tukieleza mikakati mbalimbali ya jinsi ambavyo tunataka tuhakikishe kwamba wanaotuhumiwa kesi zao zinakwenda haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mikakati mingi ya kutumia wafungwa kwa ajili ya kujiendeleza katika Jeshi la Magereza ambayo tutaizungumza baadaye; kwenye kilimo, kwenye viwanda, tunahitaji nguvu kazi. Kwa hiyo tunaamini kabisa wale ambao hawana hatia waachiwe huru, waliokuwa na hatia wafungwe ili kama hata wanaendelea kutumia rasilimali za nchi, lakini waweze kuzalisha vilevile. Kwa hiyo hakuna hata siku moja Serikali hii imekaa ikawa inapendelea kuona raia wake wanaendelea kubaki mahabusu. Jambo hili bahati nzuri tulilizungumza kwa mapana yake. Aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria, Mheshimiwa Profesa Kabudi alilizungumza akaeleza ni changamoto gani zinakabili tuhuma hizi, tuhuma za ugaidi ni kwa nini kesi zimechelewa na jitihada gani Serikali tunaingiza katika kuona mambo haya yanakwisha haraka, limeelezwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo waliniuliza, wakanipatia maandiko ambayo walieleza kwamba wao wanataka, wanaona kwamba wameshajifunza vya kutosha na kwa hiyo basi wanaomba waachiwe na kwa namna hiyo basi watakapokuwa wameachiwa hawatakubali tena kufanya siasa au kutumika kwenye siasa. Sasa nikajiuliza; kwani kesi ambayo inawakabili hawa watuhumiwa ni kesi ya siasa au kesi ya ugaidi? Ninavyofahamu ni kwamba tuhuma zile ni za ugaidi siyo za siasa, sasa unazungumza siasa imetoka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kauli hiyo ikanikaa sana kwenye kichwa na ndiyo maana ninapokuja sasa huku kwenye Bunge na maeneo mengine, naona sasa nikishabihisha na matukio yaliyotokea kipindi cha nyuma napata mashaka. Naona hapa kuna jambo lingine na kama jambo ni siasa hivi kweli Waheshimiwa Wabunge tuko tayari kuligawa Taifa hili kwa sababu ya siasa? Kama kweli hoja ni siasa na nikashabihisha baadhi ya sera za Chama Kikuu cha Upinzani kilichokuwa Zanzibar za kuendelea kudhani kwamba wataendelea kupata popularity kwa kugawa wananchi. Sera za kusema hawa Wapemba, hawa Waunguja kwamba labda watu wa Unguja wameona kwamba sera hizo hazikufanikiwa kuwaambia watu wa Unguja ambao ni ndugu za damu na wenzao wa Pemba kwamba watu wa Unguja hawawapendi Wapemba ili kupata kura tu. Au sera za kusema kwamba hawa Watanzania Bara, hawa Wazanzibari na ndiyo haya mambo ambayo yalifanyika katika kipindi cha nyuma, nikashangaa vihi dini gani ambayo inashabihisha kugawa watu? Dini gani ambayo inazungumzia masuala ya Muungano mbaya? Hivi kweli hakuna jambo hata moja zuri la Muungano? Badala ya kuwaambia wananchi watumie fursa zilizopo nyingi za Muungano, wanatumia changamoto ambazo pengine tunazikabili kila siku na kuzipunguza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikapata mashaka sana na hilo jambo na ndiyo maana nikasema kwamba yale mambo ambayo yalijitokeza kipindi kile na watu wengi ni mashahidi, tulishuhudia jinsi ambavyo baadhi ya Masheikh wengine mpake leo wana makovu na majeraha kwenye uso ya kumwagiwa tindikali, kuna Mapadre walipigwa risasi, kuna mabomu yalitegwa, ni kwa sababu ya kuendekeza na kuchanganya na yote yalifanyika kwa kutumia dini lakini kumbe leo nimegundua haya kumbe yalikuwa na malengo ya kisiasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni hatari na nimeona niyazungumze hivyo kwa mapana kwa sababu tumechoka kuona kwamba Serikali yeu inaendelea kuchafuliwa hali ya kuwa ukweli hawa wanasiasa wanaufahamu. Nataka niwahakikishie kitu kimoja tu kwamba, karne hii tuliyokuwanayo hatutakubali kuruhusu undumilakuwili wa kisiasa, hatutakubali kuona dini inatumika kujenga chuki, kujenga uadui kwa kupitia kwenye siasa. Yaliyotokea yamekuwa ni funzo kwetu sisi na ndiyo maana nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa statement nzito na muhimu sana aliyotoa Zanzibar juzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikwenda Zanzibar pamoja na tuliona kwamba kuna hatari ya kunyemelea kwa taratibu zile zile ambazo zilitufikisha pale tulipokuwepo na tukapata kazi kubwa sana na hivyo basi naendelea kusisitiza kauli ya Mheshimiwa Waziri na hii kauli ambayo aliwaelekeza Jeshi la Polisi. Kutokana na kazi za kisiasa ambazo zimeendelea kufanywa na wale wale ambao sasa wamehamia vyama vingine kwa kisingizio kwa mikutano ya ndani halafu leo wanakuja hapa wanalalamika wanasema mikutano ya ndani inazuiliwa, mikutano ya hadhara inazuiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikutano ya ndani ambayo itakuwa inafanywa kwa utaratibu kama ambavyo wamekuwa wakifanya wao kule Zanzibar, utaratibu wa kutumia mikutano ya ndani kueneza chuki, utaratibu wa kutumia mikutano ya ndani kutukana viongozi na kugawa wananchi, mikutano hiyo haitakuwa na uhalali, hata kama ni mikutano ya ndani. Mikutano ya ndani ambayo unafanya unaweka maturubai na mabomba nje na kuziba njia wananchi wasifanye shughuli zao, kupiga ngoma barabarani, kuchinja wanyama sijui mbuzi na kumwaga damu barabarani, mikutano hiyo marufuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasisitiza kauli ya Mheshimiwa Waziri kwamba kama kuna Askari ambao wanadhani kwamba baadhi yao, najua kama watakuwepo kwa Zanzibar watakuwa wachache kama wapo, kama yaliyotokea kipindi kile cha siasa na dini kwenda pamoja wakaacha mambo haya yakaenda mpaka yakafikia yalipofikia, kama wamefanya hivyo iwe kwa uzembe, iwe kwa utashi wao na mapenzi yao kwa chama chochote kile cha upinzani wachukuliwe hatua. Wasipochukuliwa hatua, wakubwa wao tutawachukulia hatua sisi na watakaokuwa nje ya mamlaka yetu tutatoa mapendekezo kwenye mamlaka husika wachukuliwe hatua. Hili jambo hatuwezi kuliruhusu, tunataka sheria ifuatwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, madhumuni ya mikutano hii najua Mheshimiwa Waziri atalizungumza, madhumuni ni kwamba sisi tunataka demokrasia hii iwe na tija kwa wananchi, demokrasia itafsiri hali halisi ya kupambana na umaskini ndiyo tafsiri ya demokrasia yetu na ndiyo maana tunasema kwamba wakati huu ni wakati wa kufanya kazi. Kwa hiyo mikutano ya hadhara inayofanywa itafanywa wakati husika. Hatuwezi tukafika hapa tukarithishana tu demokrasia za watu wengine. Wamarekani wanawake wameanza kuruhusiwa kupiga kura mwaka 1920, tokea karne na karne za nyuma zilizopita. Kuruhusiwa watu weusi kupiga kura, kushiriki uchaguzi imechukua miaka zaidi ya 100.

MWENYEKITI: Haya malizia Mheshimiwa Waziri.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tafsiri ya Demokrasia yetu ilete tija kwa wananchi na tunafanya hivyo kwa kufuata sheria kwa sababu Jeshi la Polisi linaposema kwamba linataka kuangalia intelijensia ikoje, intelijensia ni uwanja mpana. Kwa mfano; unapozungumzia intelijensia…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri malizia.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa intelijensia ya Polisi inaona kwamba sisi tunahitaji Askari wetu waende wakaangalie hali ya usalama ya wezi, hali ya usalama ya majambazi ili Wananchi watekeleze shughuli zao za maendeleo hatuwezi ku-deploy Polisi wetu wakalinda mikutano ya fujo na chuki.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Kwa hiyo tuko hapa tunasimamia kwa mujibu wa sharia, kwa hiyo tunataka Askari wote watambue hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa kumalizia; nataka nichukue fursa hii kuwaambia Askari wetu kwamba kama kuna Serikali ambayo inawapenda ni Serikali ya Dkt. John POmbe Magufuli. Katika kipindi cha muda mfupi kwa haraka haraka, toka Serikali ya Dkt. Magufuli imeingia madarakani kuna mambo makubwa Jeshi letu la Polisi limefanyiwa ambayo ni ya kutolea mifano na hayajafanyika kwa miaka mingi nitataja machache:-

Mheshimia Mwenyekiti, mafao ya wastaafu ni moja ya changamoto kubwa kwa Askari wetu na takwimu hapa zinaonesha ni kwa kiasi gani tumefanikiwa. Masuala ya ucheleweshwaji wa mishahara kwenye vyeo ilikuwa ni changamoto kubwa kwa Askari wetu, sasa hivi mambo haya yamepata ufumbuzi kwa kiasi kikubwa sana. Mheshimiwa Waziri wa Utumishi amezungumza, tunatarajia kupandisha vyeo vingine zaidi mwaka huu wa fedha pamoja na kuajiri askari wapya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, posho mbalimbali ziko katika hatua za kuongezwa, mpaka hata sasa makazi ya Askari yanaboreshwa. Serikali hii ya Dkt. Magufuli inaimarisha vitendeakazi ikiwemo vyombo vya usafiri na teknolojia za kisiasa kwa ajili ya matumizi ya Jeshi la Polisi. Hali kadhalika, katika masuala…

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: …ya mafunzo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Msigwa kaa.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: …masuala ya mafunzo pamoja na…

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Msigwa kaa kwanza

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: …Serikali hii imeangalia kwa karibu sana. Kwa hiyo hoja za Wapinzani hazina mashiko. Serikali hii…

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Waziri ahsante wka mchango mzuri, ahsante nimekuongeza dakika saba.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii lakini pia nikupongeze kutokana na kazi kubwa na nzuri ambayo unaifanya katika Bunge hili pamoja na wasaidizi wako wote.

Mheshimiwa Spika, lakini pili nichukue nafasi hii kwa mara nyingine tena kumshukuru sana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuwa na imani na mimi lakini pamoja na kuweza kutuongoza vizuri na kutusimamia vyema katika kutekeleza majukumu yetu pamoja na Mheshimiwa Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango Waziri wangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, kwa kweli ananisaidia sana katika kutekeleza majukumu yangu. Mimi na yeye tofauti yetu ni moja ndogo ya kishabiki, lakini ni mtu ambaye tunafanya naye kazi vizuri toka Mambo ya Ndani na sasa tunaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nishukuru sana watendaji wote wa Wizara ya Fedha na Mipango nikianzia na Katibu Mkuu, Manaibu Katibu Mkuu, Makamishna wakurugenzi na wakuu wa Taasisi mbalimbali zilizopo katika Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani hizo naomba sasa niende moja kwa moja kwenye hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge walizungumza. Hoja ya kwanza niliomba nichangie inahusu mfuko wa pamoja wa fedha ambao Kamati ya Bunge pamoja na baadhi ya waheshimiwa Wabunge walizungumza kuonyesha concern yao ni kwamba sasa imekuwa muda mrefu sana, mfuko huu haujaanzishwa.

Mheshimiwa Spika, nataka nichukue fursa hii kupitia kwako kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge pamoja na Kamati kwamba kimsingi suala la mfuko la pamoja wa fedha ni matakwa ya Kikatiba, na kama matakwa ya kikatiba basi utekelezaji wake ni jambo ambalo linapaswa liendelee kuzingatia misingi hiyo ya kikatiba na mpaka sasa hivi kuna hatua kadhaa ambazo zilizofanyika. Kwa sababu tayari mfuko wa pamoja wa fedha kwa maana ya Joint Finance on Committee imeshaundwa na kupiata Joint Finance on Committee kuna hatua mbalimbali ambazo zimechukuliwa za kuanzisha mfuko huo pamoja na fedha.

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa hatua hizo ni kwanza kwa sababu jambo lenyewe ni kubwa sana lilihitaji kufanya utafiti wa kina kuona ni jinsi gani ambapo mfuko huu utaweza kusimamiwa vizuri na uweze kuleta tija na kuwa endelevu mpaka sasa stand nyingi zimefanyika na zimekamilika, lakini pia hali kadhalika hatua ambayo imefikiwa mpaka sasa hivi iko katika hatua ya maamuzi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni hakikishe Waheshimiwa Wabunge kwamba sisi tutahakikisha tunasimamia katika hatua za mwisho zinazobakia ikiwemo kuandaa waraka kwa ajili ya kupeleka kwenye mamlaka za juu kwa ajili ya kufanya maamuzi. Mahamuzi hayo yatakapokuwa yamefikiwa basi ni imani yangu kwamba mfuko huu utaweza kuanza kufanya kazi ni jambo ambalo ni la msingi nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge pamoja na Kamati lakini ni jambo ambalo vile vile tunalichukua kwa uzito unaostahili.

Mheshimiwa Spika, lakini katika hili baadhi ya wachangiaji walizungumzia kuhusiana na hoja ya changamoto ya VAT, nadhani Mheshimiwa Mbunge Ali King alizungumza kuhusiana na changamoto hiyo. Nataka nimhakikishie kwamba kwanza ni kweli mfuko huu ni muhimu lakini si kweli mfuko huu unaweza ukazitatua changamoto hiyo ya VAT ambayo ni mezungumzwa.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya mujibu wa Katiba yetu kuna kodi ambazo zimezungumzwa kuwa ni kodi za Muungano, ikiwemo Kodi ya Mapato ambayo inalipwa na watu binafsi, mashirika, pamoja na ushuru wa forodha, pamoja na ushuru wa bidhaa. VAT moja kati ya kodi za Muungano.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, nataka niwahakikishie kwamba changamoto hii na yenyewe tumeifanyia kazi kwa sababu Mheshimiwa Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar hivi karibuni pamoja na timu yake walikuja tukafanya nao mazungumzo na kuna mambo ambayo tumekubaliana lakini kwa sababu bado bajeti haijaiwasilisha Mheshimiwa Waziri namuomba Mheshimiwa Mbunge avute subira ninauhakika Mheshimiwa Waziri, wakati ambapo atakuja kuwasilisha bajeti yake atakuja kulizungumzia na kulitoalea ufafanuzi suala hili kwa kina kabisa.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo jingine ambalo nilitaka kulichangia ambao Waheshimiwa Wabunge wengi wamelizungumza ni juu ya hofu yao kubwa ambayo ni ya msingi kabisa walioyokuwa nayo ya juu ya riba kubwa kwenye mabanki yetu ambayo imeathiri sana uwekezaji katika nchi hii. Ni Dhahiri kabisa riba kubwa katika mabenki ya biashara inachangia sana kuzorotesha kasi ya uzalishaji katika viwanda, lakini vile vile inasababishwa kupunguza dhamira ya Serikali ya kuweza kuona ina ajiri watu wengi Zaidi kupitia katika uwekezaji mbalimbali ikiwa kwenye viwanda, ikiwa kwenye biashara na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, lakini pia inachangiwa vile vile kupunguza fursa za Serikali za kukusanya kodi. Kwa hiyo, ni hoja ambayo ni ya msingi kwa hiyo ni hatua nyingi ambazo banki ya Tanzania imechukua ambazo zimesaidia ama ziko zinalenga kuhakikisha kwamba banki zetu za biashara zinatoa riba nafuu kwa wananchi wake. Miongoni mwa hatua hizo kupitia sera yetu ya fedha imeweza kuhakikisha kwamba inaongeza ukwasi katika mabenki haya.

Mheshimiwa Spika, lakini jingine ambalo BoT imechukua hatua kuhakikisha kwamba inapunguza riba za BoT kwenda katika mabanki mengine kutoka asilimia 12 mpaka asilimia tano. Lakini hali kadhalika hatua nyingine ambazo nimezichukua kuhakikisha kwamba inapunguza viwango vya amana kutoka asilimia 8 mpaka asilimia 6.

Mheshimiwa Spika, lakini kwamba hiyo haitoshi hali kadhalika BoT imeendelea kuboresha mfumo wa taarifa za wakopaji ili kuhakikisha kwamba mabenki yetu yanatambua wale ambao wakopaji ambao wako katika kiwango cha high risk. Lakini mambo mengine ambayo umechukua kama hatua za kuhakikisha kwamba kodi riba inapungua katika mabenki ili mabenki haya yaweze kukopesha kwa riba ya chini.

Mheshimiwa Spika, lakini hata hivyo bado kuna masuala ya kujiuliza juu ya jitihada zote ambazo benki yetu ya Tanzania imechukua lakini bado riba ziko juu haziridhishi. Nataka nikubaliane na Waheshimiwa Wabunge kwamba hoja hii ni hoja ya msingi na vile vile haikubaliki kwa sababu kuna mambo ambayo mabenki ya biashara yatakuwa lazima yatueleze kwamba mbali ya jitihada hizi ambazo benki ya Tanzania imechukua wenyewe wamefanya jitihada gani kuhakikishwa wanakabiliana na changamoto hii kubwa riba. Kwa sababu madhara ni makubwa yanapunguza na kudhorotesha kasi ya maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, malengo ya Serikali ni kuhakikisha kwamba riba hizi zinashuka. Sasa hili riba nyingi katika mabanki zinatoka katika asilimia 12 kwenda juu, tunachokitaka ziwe chini ya asilimia 10. Kwa hiyo, nataka niseme kwamba katika hili lazima tukubaliane na Waheshimiwa Wabunge kwamba tutahakikisha kwamba tunafanya jitihada za ziada ili tuchukue hatua za ziada kuzisimamia hizi benki hizi za biashara ziweze kupunguza riba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na moja katika mambo ambayo tunayachukua tutayaelekeza BoT kuhakikisha mara baada ya kikao hiki cha bajeti kuweza kukaa na wadau wote ikiwemo mabenki ya biashara ili kuzungumza nao wadau hawa kuwasikiliza waweze kujua ni jambo gani ambalo linapelekea kufanya wao washindwa kushusha riba hizi chini ya kiwango cha angalau asilimia 9 kushuka chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge kwa kufikiria jambo hilo lakini niwahakikishie kwamba tumechukua mawazo yenu na tunaanza kuyafanyia kazi kwa mkakati huo ambao nimeueleza. Naamini kabisa tukisimamia vizuri na tukiwasikiliza tunaweza kufika hatua nzuri na malengo ya Serikali ya kuhakikisha kwamba wananchi wanapata mikopo kwa riba za kiwango chenye kuridhisha yanafikiwa.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo imezungumzwa na baadhi ya Wabunge kama mapendekezo ni kupunguza rate za hati fungani kutoka asilimia 15 kuja chini ya asilimia 15. Kwanza, niseme kwamba mpangilio wa rate za hati fungani uliopo sasa hivi unategemea na miaka, ziko hati fungani ambazo rate yake inafika mpaka asilimia 7.2 zile ambazo zinachukua miaka miwili, hii asilimia 15 ni ya miaka 25.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo wazo la Waheshimiwa Wabunge tumelichukua ingawa wazo hili linahitaji kuangaliwa kwa umakini sana, kwa sababu kupunguza hati fungani ziwe za kiwango cha chini zaidi kunaweza kuathiri uchumi na kufanya hati fungani zile zikakosa soko. Kwa hiyo, kuna mambo mengi ambayo inabidi tuyaangalie kabla ya kuizingatia hoja hii ambayo Waheshimiwa Wabunge wametoa. Naamini kwamba ni wazo zuri tumelipokea na tutalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kuchangia ni suala la ukusanyaji wa mapato. Waheshimiwa Wabunge wengi wameshauri jinsi ya kufanya ili tuweze kukusanya mapato vizuri Zaidi. Nichukue fursa hii kuipongeza sana Mamlaka ya Mapato (TRA) kwa kazi nzuri ambayo imefanya mpaka sasa hivi toka Serikali ya Awamu ya Sita imeingia madarakani.

Mheshimiwa Spika, kuna takwimu ambazo zipo zinaonyesha kuwa tumepiga hatua ya kuridhisha. Kutokana na mabadiliko makubwa ambayo tumeyafanya kwa kipindi kifupi tungetarajia pengine tungetetereka katika ukusanyaji wa mapato lakini hali haikuwa hivyo. Kwa mfano, katika takwimu ambazo tumezipokea za Machi mpaka Mei hii malengo ya ukusanyaji wa mapato yameongeza kulinganisha na kipindi cha miezi ya nyuma. Kwa hiyo, hizi ni jitihada kubwa sana ambazo zimefanyika na zinahitaji kupongezwa.

Mheshimiwa Spika, haya yamefanyika kwa sababu kuna mambo ambayo TRA wamefanya. Moja, imehakikisha kwamba inaongeza weledi katika ukusanyaji wa mapato. Pili, kujenga mazingira mazuri ya biashara. Haya ndiyo malengo ambayo sisi tumeyapanga katika Serikali na mimi nawapongeza TRA kwa kuanza kuyasimamia vema mapema kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kuhakikisha kwamba weledi huo unapotumika unahakikisha unajenga mazingira mazuri ya walipa kodi kulipa kodi kwa hiyari badala ya kutumia ubabe. Kwa hiyo, ndiyo mambo ambayo kimsingi yamesaidia kufanya mapato yetu kukua. Nina takwimu hapa lakini kutokana na muda nisingependa kuzisoma, lakini takwimu hizi zipo wazi kupitia TRA zinapatikana kila mtu anaweza akaona jinsi ambavyo tumepiga hatua katika miezi hii mitatu toka Serikali ya Awamu ya Sita imeingia madarakani mbali ya kufanya reform za aina nyingi ambazo nimezieleza na nyingine ambazo sijazieleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mambo hapa Waheshimiwa Wabunge wameshauri na mimi nasema ni ya msingi. Moja, wanazungumzia kuhusu eneo hili la mifumo; ni kweli tuna changamoto ya mifumo, ni dhahiri mifumo hii inachangia katika kupunguza kasi hii ya ukusanyaji wa mapato. Kwa mfano, sasa hivi tunategemea kodi kubwa katika maeneo makubwa matatu; ushuru wa forodha kupitia bandari, walipaji wa kodi wakubwa lakini kuna eneo kubwa sana la kodi za ndani ambalo hatujafanya vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, eneo hili na mengine tunaweza kufanya vizuri zaidi ikiwa tutayazingatia maoni ya Waheshimiwa Wabunge ambayo kimsingi tumeshaanza kuyafanyia kazi. Moja, ni eneo la mifumo kuhakikisha inakuwa harmonized na inasomana. Nataka kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba tupo katika hatua za kuhakikisha kwamba tunaboresha na kuimarisha mifumo yetu pale TRA ili tuweze tuwe na mifumo ambayo itakuwa inafanya kazi vizuri ya kuweza kusimamia mapato. Hii itasaidia vilevile kupunguza rushwa kwani itasaidia kupunguza makutano baina ya walipakodi pamoja na wasimamizi wa kodi.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo Waheshimiwa Wabunge wamelizungumza na ni la msingi hasa inapokuja hoja ile ya block management ambayo inahitaji rasilimali watu. Kwa hiyo, niwahakikishie kwamba tuna dhamira hiyo na tunashirikiana na Idara ya Utumishi ili kupata kibali cha kuajiri watumishi wa TRA wa kutosha. Sasa hivi tuna watumishi ambao hawazidi 5,000 lakini tukipata watumishi angalau 1,000 basi tunaweza tukapiga hatua nzuri zaidi. Niwahakikishie kwamba kwa kushirikiana na mamlaka nyingine za Serikali tutafanya kila linalowezekana hali itakaporuhusu tuweze kuongeza idadi ya watumishi TRA pamoja na kuimarisha mifumo yetu ili haya mafanikio ambayo tunayazungumza yaweze kuzidi mara dufu au zaidi ya mara dufu ya tunayojivunia leo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine ambalo napenda kulizungumza ni hoja hii ya PPP. Tumezungumza hapa wakati wa Mpango kwamba moja ya vipaumbele vya Serikali hii ni kuhakikisha kwamba nafasi ya private sector inachukuwa umuhimu mkubwa kushiriki kwenye uchumi wa nchi hii. Hili litafanyika kupitia utaratibu wa foreign directly investiment ama kupitia kwa utaratibu wa wawekezaji wetu wa ndani ama kupitia utaratibu wa ubia katika sekta ya umma na sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, kuna hatua kadhaa ambazo zimeshachukuliwa; tuna sheria nzuri lakini kuna jambo ambalo lazima tukubaliane kwamba tunatakiwa tulifanye kwa haraka, tunahitajika kuhakikisha tunaanzisha PPP center kwa haraka. Hili Waheshimiwa Wabunge tunaahidi kwamba tutalikamilisha muda si mrefu. Imani yetu tukianzisha taasisi hii itasaidia sana kuharakisha na kuwa kiunganishi muhimu kati ya wawekezaji pamoja na taasisi za umma lengo ni kuona nafasi ya miradi ya PPP inakuwa kwa haraka na inaimarishwa. Katika hili niwahakikishieni kwamba tutakwenda nalo vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini lingine ambalo wamelizungumza wamesema kwamba kuna haja ya kupunguza mitaji kutoka dola za Marekani milioni 20 mpaka kuwa Dola milioni 5 mpaka 10.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante, malizia tu hilo.

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita katika maeneo matatu. Nitazungumzia suala la madawa ya kulevya lakini nitazungumzia hali ya usalama hasa Zanzibar na muda ukipatikana nitamalizia na suala la magereza. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka nilieleze Bunge hili Tukufu kwamba kuna kazi kubwa sana ambayo Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikiifanya, imefanya na inaendelea kufanya katika kukabiliana na janga hili la madawa ya kulevya katika nchi yetu. Yapo mambo yameendelea kufanyika waziwazi na yapo mambo ambayo yamefanyika kimya kimya hayajulikani na mengine hayatajulikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika haya mapambano ya dawa za kulevya, nataka niwahakikishie kwamba tunaendelea vizuri na imani yangu ni kwamba kwa mwelekeo huu tunaoenda nao tunaelekea kushinda na hatutarudi nyuma. Silaha yetu kubwa ni dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli. Wewe na Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi wakati Mheshimiwa Rais alivyokuja kuzindua Bunge hili alizungumza kwa msisitizo na toka wakati ule mambo mengi na makubwa yamefanyika. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hoja ya msingi ni kwamba tumefanikiwa kiasi gani, changamoto ni zipi na tunaelekea wapi. Tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa sana, ni watumiaji na wauzaji wa madawa ya kulevya wakubwa, wa kati na wadogo wengi ambao wamekamatwa na wengi kesi zao zinaendelea na wapo wengi ambao wameshafungwa. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lazima tukiri kwamba kulingana na mabadiliko ya mfumo wa kidunia zamani nchi yetu ilikuwa inatumika kama ni eneo la kupitishia madawa ya kulevya lakini sasa hivi ongezeko la matumizi ya ndani la madawa ya kulevya limekuwa ni kubwa. Madawa ya kulevya yanatumika hovyo, hilo lazima tukiri kama ni changamoto. Changamoto hii Serikali hatuwezi tukaifumbia macho na ndiyo maana tumebadilisha style ya kukabiliana na matatizo ya madawa ya kulevya. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tu hapa katika ziara zake nyingi Mheshimiwa Waziri ambazo amekuwa akifanya mara ya mwisho alikuwa Ifakara amezungumzia hilo, ametoa mwelekeo huo na mimi nilikuwepo Mbeya takribani wiki mbili zilizopita kabla hata ya operesheni moja haijafanyika ikiwemo ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam. Tumewaelekeza ma-RPC kwamba kwa uzito wa tatizo la madawa ya kulevya katika nchi yetu, tuliwaelekeza Mbeya tukawaambia wafanye operesheni kabambe kabisa na wakafanya operesheni kali sana wakawakamata watumiaji wa madawa ya kulevya na wauzaji. Wale watumiaji wa madawa ya kulevya ndiyo waliotusaidia kuweza kuwapata wale ambao wanashughulika na kuuza madawa ya kulevya. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, tulidhamiria kwamba tutumie utaratibu huo ili kuweza kupata taarifa na kuukamata mtandao mzima wa madawa ya kulevya na hatimaye kuangamiza na kupunguza matumizi makubwa ya madawa ya kulevya yaliyopo mitaani. Jambo hilo limefanyika kwa mafanikio makubwa sana kwa upande wa Mbeya peke yake watu zaidi ya 17 ambao walikuwa either wanatumia au wanauza madawa ya kulevya walikamatwa na kesi zao wengine zinaendelea. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hakika Wakuu wa Mikoa ambao ni Wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama wa Mikoa yao ikiwemo Mkoa wa Mbeya wameendelea kusimamia hilo na mikoa mingine ikiwemo Dar es Salaam na Shinyanga na kadhalika. Kwa hiyo, tunataka tulihakikishie Bunge hili Tukufu kwamba vita hii ni vita ambayo hatutarudi nyuma na tunaomba ushirikiano wa wananchi na Waheshimiwa Wabunge waliomo humu kuweza kuhakikisha kwamba tunaimaliza. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni suala la usalama wa nchi yetu. Naomba nigusie mambo madogo mawili kwa sababu ya muda. Kumekuwa kuna hoja ya mashaka kuhusiana na majibu ambayo tunatoa kuhusu hali ya ugaidi katika nchi yetu. Naomba nirudie tena kwamba nchi yetu hakuna ugaidi bali kuna vimelea vya ugaidi. Vimelea hivi vya ugaidi havijafanikiwa kuzaa matukio makubwa ya ugaidi kwa sababu ya kazi kubwa ya vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ambayo vimeendelea kufanya katika nchi hii. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiachia tukio moja ambalo limewahi kutokea katika miaka ya nyuma ya ulipuaji wa Ubalozi wa Marekani lakini mpaka sasa hivi tumeweza kudhibiti kwa kiwango kikubwa sana. Kwa hiyo, msimamo wa Serikali ndiyo huo, msimamo wa Wizara ya Mambo ya Ndani ndiyo huo na msimamo wa Wizara ya Katiba na Sheria kama alivyozungumza Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe ni hivyo hivyo hakuna mgongano wowote katika hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ambalo limezungumzwa sana ni suala zima la hali ya usalama Zanzibar, tusichanganye vitu. Tulichokizungumza ni taarifa ambayo imekuwa ikiletwa hapa na Wabunge mbalimbali, wengine wamekuwa wakisambaza picha kwenye Facebook wakichukua watu wengine hatujui walikuwa wanaumwa malaria au kitu gani wakisema tumepigwa na watu ambao wanaitwa Mazombi. Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunasema kwamba Zanzibar hali ya usalama ni shwari na Tanzania hali ya usalama ni shwari. Hata hivyo, kwa kusema hivyo, hatuna maana kwamba hakuna element za uhalifu, wezi, walevi wanaokunywa pombe haramu watakuwepo na kadhalika. Hao watu ambao wanaitwa Mazombi sisi tumesema kabisa kwamba kama kuna mtu yeyote ana taarifa ya watu hawa aiwasilishe katika vyombo vya dola. Mpaka sasa hivi hakuna mtu yeyote ambaye amewasilisha taarifa hii rasmi katika vyombo vya dola na ndiyo maana msimamo wetu unaendelea kubaki pale pale kwamba taarifa hizo kama Serikali hatuna. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa haraka haraka kuzungumzia suala la magereza. Kuna mambo makubwa matatu ambayo tunayasimamia kwa nguvu zetu zote. Jambo la kwanza, kama Mheshimiwa Rais alivyosema kwamba wafungwa wafanye kazi tumelisimamia hilo kwa mafanikio makubwa. Leo tunavyozungumza tumpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa fedha shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Askari Magereza Ukonga. Katika ujenzi ule tumetumia wafungwa na tumefanikiwa kuokoa fedha ambazo zimewezesha kujenga zaidi ya nyumba 80. Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kana kwamba hiyo haitoshi matumizi ya wafungwa yametusaidia sana katika kuweza kufanya kazi mbalimbali za ujenzi katika magereza yetu. Katika Wilaya na Nkasi kulikuwa kuna changamoto sana ya mahabusu. Tulifanya ziara huko hivi karibuni na hivi tunavyozungumza ni kwamba shughuli za ujenzi wa mahabusu katika Wilaya ya Nkasi zinaanza kwa matumizi ya nguvu kazi za wafungwa… (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kuunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii ya kuweza kutoa mchango wangu kuhusiana na bajeti hii ya mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Spika, aidha nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa mwongozo wake aliotupatia tukaweze kuwasilisha bajeti hii ya aina yake, bajeti ambayo imegusa wananchi na bajeti ambayo Waheshimiwa Wabunge wameiunga mkono kwa kiwango cha hali juu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nichukue fursa hii vilevile kuipongeza sana Kamati ya Bajeti ya Bunge lako Tukufu chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Daniel Sillo na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Omari Kigua na Wajumbe wote wa Kamati hii, pamoja na Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa michango yao mizuri sana ambayo imesaidia sana katika kufanya tuweze kuwa na bajeti ambayo tutaikamilisha leo Mheshimiwa Waziri atawasilisha majumuisho yake ya ufanisi wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nianze kwenda moja kwa moja kwenye baadhi ya hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezichangia; hoja ya kwanza ambayo nilitaka kuizungumzia leo ni ufafanuzi wa hoja ambayo Waheshimiwa Wabunge wameizungumzia baadhi yao kuhusu miamala ya simu kwa upande wa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, wapo Wabunge ambao walitaka kuona kwamba fedha hii ambayo inakusanywa kwa malengo mema kabisa, je, fedha hii ambayo inatozwa kodi kwa wananchi wote wa pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini mipango ya matumizi yake haijagusa miradi ya maendeleo ya kijamii kwa upande wa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kabla ya kutoa ufafanuzi huo naomba niseme neno moja kwa ufupi sana, Muungano wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni muungano wa damu na ni muungano wa kindugu, si muungano wa vitu au maslahi hata waasisi wa Taifa hili kilichowashawishi na kuwafanya waweze kuunganisha nchi hizi mbili ni historia ya udugu wa damu baina ya pande hizi mbili tokea wakati kabla ya ukombozi wa nchi hii mpaka hivi sasa na haikuwa kwa sababu ya maslahi kwamba nani atapata nini na nani atafaidika na nini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini wakati kila miaka ikielekea mbele na vizazi vinavyoendelea kuzaliwa na sisi wazee ndiyo tunamalizika malizika, basi utaona kwamba hii dhana inaanza kupotea uelewa wake na ndiyo maana wazee hawa waliamua kwa makusudi kabisa kuweka kwenye Katiba kuanzisha Mfuko wa Pamoja wa Fedha. Dhamira yake ni hiyo hiyo kuweza kubaini mapato na matumizi ya Muungano ili yaweze kutumika kwa mujibu wa Katiba.

Mheshimiwa Spika, lakini wakati mchakato huo unaendelea kama ambavyo tumeahidi wakati tunawasilisha bajeti ya Wizara siku chache zilizopita, hivi sasa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuna baadhi ya mapato yake ambayo inaruhusiwa kukusanya yenyewe na hivi majuzi tu mliona Mheshimwia Waziri alivyozungumzia kwenye bajeti yake kuhusiana na mapato yanayohusu uhamiaji, kwa maana hiyo basi hatuoni tatizo lolote kwenda sambamba na mawazo ya Waheshimiwa Wabunge na hivyo tumewapa wataalam kazi ya kuchambua matumizi haya ili pale zitakapokusanywa, zile fedha ambao zitakusanywa kwa Zanzibar ziweze kupelekwa Zanzibar, zitumike kwa ajili ya maendeleo ya Zanzibar kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaamini kabisa kwamba tukifanya hivyo tutaweza kupanua ile dhana nzima ambayo tumekuja nayo ya kuhakikisha kwamba kila mtu analipa kodi na anafurahia hayo maendeleo ya kodi yake kwa sababu madhumuni ya kodi hii ni kugusa huduma za jamii, kodi hii ama tozo hizi zinagusa maisha ya watu watu moja kwa moja katika sekta zote za kijamii muhimu ikiwemo afya, elimu na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo limezungumzwa vile vile ni ile hoja ya kwamba taarifa ya ambazo zinatoka BOT kwenda masharika ya kimataifa hazina taarifa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, BOT ni chombo cha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, taarifa za kifedha zote ikiwemo sera ya fedha pamoja na taarifa zingine zote zinahusisha ama zinazingatia upekee wa Zanzibar kwa uchumi wa Zanzibar. Lakini hoja ya taarifa zinazotoka World Bank na yenyewe tunaona ni ya msingi. Hivyo basi kwa kuanzia tumeamua kwamba tutawashawishi Benki ya Dunia wafungue ofisi yao Zanzibar ili kuweka karibu na kuweza kutatua tatizo hili kwa siku zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo mambo mengi ambayo yamefanyika kurekebisha zinazoitwa changamoto za Muungano na tumeweza kwenda nazo vizuri tu, hata hili ambalo Wabunge wengi wamelalamikia kuhusiana na changamoto ya magari ambayo yanakuwa registered Zanzibar kutokufanya kazi upande huu naamini kabisa muda si mrefu, Mheshimiwa wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwa wakati ambao ataona unafaa na kama utaratibu zitakazokua zimekamilika za Kiserikali hataleta mabadiliko ya Sheria ya Usalama Barabarani ambayo yataondoa moja kwa moja tatizo hili na kulipatia ufumbuzi wa kudumu. Kwa hiyo, kwa hayo makubwa tumemaliza hatuwezi kushindwa na hili dogo.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ninalota kulizungumza ni changamoto ya upatikanaji wa mikopo nafuu kwa ajili ya utekelezaji wa miradi; mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha tunatumia rasilimali zetu vizuri ili tuweze kujitegemea, huo ndiyo mwelekeo wa msingi kabisa na ndiyo maana ukiangalia katika bajeti hii ni bajeti ambayo katika kipindi cha miaka kumi imeweza kuja na utegemezi mdogo wa asilimia 8.1 kutoka kwa wahisani, lakini ni lazima tukope ili tuendelee kama ambavyo walioendelea wanaendelea kukopa. Lakini cha msingi mikopo hii ambayo tunakopa tunataka tuhakikishe kwamba inaendelea kulengwa katika miradi ya maendeleo ambayo inachochea uchumi wa nchi hii. Lakini tuhakikishe mikopo hii inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kuepuka mazingira yote ya ubadhilifu na wizi wa fedha hizi.

Mheshimiwa Spika, sasa katika kufanya hivyo Serikali yetu hii ya Awamu ya Sita imeendelea kuhakikisha kwamba inaimarisha mahusiano na Jumuiya ya Kimataifa na ninyi mashahidi kwa kipindi kifupi toka Mama Samia ameingia madarakani ameweza kuimarisha mahusiano ya kimataifa na tumeweza kupata mikopo yenye masharti nafuu ya zaidi ya dola 1500 kwa kipindi kifupi na mikopo hii ya masharti nafuu ni muhimu sana ili kwanza kuhakikisha tunalinda maadili na heshima na uhuru wetu, lakini vilevile tunapata mikopo haiwi mizigo kwa wananchi wa nchi hii yenye riba nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mikopo hiyo zaidi tunalenga kama ambavyo Kamati na Waheshimiwa Wabunge mmeshauri ni mikopo ile ya concessional loans na semi concessional loans ambao vilevile ina element ya grant ndani yake na masharti yake yanaridhisha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na hoja deni tunaendelea kukopa haliyakuwa tukiji-proud kwamba deni letu ni himilivu, kwa sababu ukiangalia takwimu mpaka Desemba, 2020 uwiano wa deni la mapato ya ndani ni asilimia 13.7 wakati ukomo ni asilimia 23; kwa hiyo tuko vizuri, ziko nchi majirani zetu wanakaribia kufika kwenye ukomo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini maoni yenu kuhusiana na mchakato wa sovereign credit rating tumechukua na tunafanya kazi kama ambavyo tume ya Mheshimiwa Waziri imeelezwa na vilevile tutaendelea ku-maintain ukopaji wa ndani wa chini wa kiwango cha asilimia moja ya pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo imezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge ni kuhusiana na projection ya asilimia 5.6 ya ukuwaji wa uchumi kwamba ni ndogo sana. Projection hii imezingatia nadharia nzima ya hali ya ulimwengu wetu na mazingira yaliyonayo sasa hasa katika kipindi ambacho ulimwengu umekumbwa na janga la UVIKO 19. Hali hiyo imesababishwa hata uchumi wa dunia na wenyewe ukuaji wake projection yake iwe kwa asilimia sita kwa mwaka unaokuja, ingawa inatarajiwa vilevile mwaka 2022 kurudi katika kiwango cha asilimia 4.4 almost kiwango cha kawaida.

Mheshimiwa Spika, ukuwaji wa uchumi wa nchi zilizopo chini ya Jangwa la Sahara wenyewe unakadiriwa kuwa kwa asilimia 3.4. Kwa hiyo, sisi makadirio yetu asilimia
5.6 yamezingatia mazingira mazima ya hali ya uchumi wa dunia ingawa maoteo yetu kwa miaka mitano inayokuja kama ambavyo mpango unaeleza ni kufikia kiwango cha asilimia nane.

Mheshimiwa Spika, tumeweka mazingira mazuri na misingi mizuri katika bajeti hii ili malengo ya asilimia nane yaweze kufikiwa na mambo haya ambayo tumefanya miongoni mwao kwanza ni kuhamasisha matumizi ya malighafi zetu za ndani ili kuongeza mnyororo wa thamani, lakini pia kuimarisha miundombinu wezeshi hususani sekta ya usafirishaji kwa maana ya barabara, reli, viwanja vya ndege, bandari halikadhali nishati na umemelakini kuhakikisha tunaimarisha uwekezaji na biashara wa sekta binafsi tunaamini kabisa mambo haya ndiyo msingi ya bajeti yetu tukiyasema vizuri ongezeko la ukuaji wa uchumi kwa asilimia nane kwa miaka mitano inayokuja tutaufikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine la kuzingatia na lamsingi kabisa ni kwamba katika bajeti hii tumetenga asilimia 37 ya bajeti kwenye maendeleo ambayo yanachochea ukuaji wa uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa mengine ambayo nilitaka niyazungumze kwa haraka haraka kuna hoja kadhaa ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezungumza ikiwemo hoja hii ETS, lakini vilevile kulikuwa na hoja ya gypsum pamoja na hoja ongezeko la kodi kwa matrela haya.

Mheshimiwa Spika, nimebahatika kuongoza kikao kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri ambacho kilihusisha baadhi ya malalamiko mengi ambayo yalijitokeza kuhusiana na hii suala ya ETS, kwa hiyo, hatua ambayo tulichukua tuliona kuna umuhimu wa kuzikutanisha pande zote ili tuweze kujua, kusikiliza hoja za pande zote mbili na kutoa maamuzi sahihi. Katika kikao hicho ambacho mimi ndiye nilikuwa Mwenyekiti wake tulikubaliana yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza; tumekubaliana kwamba hoja ya Waheshimiwa Wabunge kuhusiana na ukubwa wa gharama wa ETS ni sahihi, lakini tumekubaliana kwamba matumizi ya teknolojia hii ni muhimu sana katika kuhakikikisha kwamba tunadhibiti mapato ya Serikari. (Makofi)

Kwa hiyo maelekezo ambayo tumetoa ni kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuweza kukutana na wadau hawa ili kufanya majadiliano ikiwemo pamoja na mambo mengine kuangalia uwezekano wa kuweza kushusha gharama hizi ambazo zinalalamikiwa ambao ni mzigo kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wakati hilo linaendelea hali kadhalika tumewaelekeza Mamlaka ya Mapato Tanzania kujipanga ili siku zijazo zoezi hili waweze kulifanya wenyewe. (Makofi)

Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge kana kwamba hiyo haitoshi kwa kuzingatia umuhimu wa jambo hili tumekubaliana kwamba kuna haja ya kufanya upembuzi yakinifu unaojitegemea ili kubaini kwa undani kabisa masuala yote yanayohusu utekelezaji wa mradi huu na jambo hilo litasaidia kuweza kutupa mwongozo wa baadaye wa kuweza kutoa maamuzi sahihi ikiwemo wakati wa majadiliano ya kibiashara pamoja na wawekezaji wanaohusiana na biashara ama hata ikifika mahali tumeweza wenyewe kufanya basi tuwe tunaweza kufanya tukiwa tuna taarifa ambazo za kitalaam na zimethibitishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna mambo ambayo mengine yamezungumzwa niseme tu kwa ufupi ni kwamba tumeyapokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge na yale ambayo pengine kutokana na muda hatuwezi kuyaeleza najua Mheshimiwa Waziri ataeleza mambo mengi, lakini kwa sababu mambo ambayo yamezungumzwa ni mengi na hatutaweza kuyamaliza yote kwa leo.

Mheshimiwa Spika, tuhakikishie kwamba tumeyachukuwa na tutazingatia maoni ya Waheshimiwa Wabunge ikiwemo mambo haya mawili ambayo sikupata muda wa kuyazungumzia ya ile hoja ya gypsum pamoja na ongezeko la kodi ya ushuru wa forodha kwenye matrela, lakini tutayachukulia hatua kwa mujibu wa maelekezo na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ENG. HAMAD MASAUNI YUSSUF: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianze kwanza kuipongeza Serikali kwa ufanisi wa utekelezaji wa Mpango wa Miaka Mitano iliyopita ambao tumeona mwenendo wa viashiria vyote vya uchumi vikiimarika licha ya nchi yetu ama dunia kwa ujumla kukumbwa na janga la Covid 19.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mtazamo wangu mafanikio haya yamechangiwa zaidi na uongozi imara, uongozi thabiti na wenye maono katika nchi yetu. Mara nyingi uongozi thabiti na uongozi imara hupimwa pale Taifa linapoingia katika misukosuko ama Taifa linapohitajika kutoa maamuzi magumu na mazito kwenye maslahi ya nchi na watu wake hapo ndio unaweza kujua kama nchi hii ina uongozi thabiti ama laa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi bahati njema Mheshimiwa Dkt. John Magufuli, kiongozi wetu mkuu amejipambanua vya kutosha katika eneo hilo, wala sio nilichokipanga kukizungumza hapa. Leo nimepanga kuzungumza mchango wangu kuhusiana na mpango. Nitaomba angalau nitumie hata dakika moja nizungumze jambo moja la msingi sana na hasa kwa sisi ambao tunatokea Zanzibar. Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli wakati akiwa vilevile ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi amesimamia vema maandalizi ya ilani ambayo maandalizi hayo katika Ibara 136(e) kwenye maeneo mahususi ya Zanzibar yameweza kutoa mwelekeo mpya wa uchumi wa blue kama ni sekta ya kipaumbele kwa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichukue fursa hii kumpongeza sana Rais wa sasa hivi wa Zanzibar, Mheshimiwa Dkt. Hussein Mwinyi ameanza vizuri sana katika siku si zaidi ya mia moja tumeshuhudia utiaji saini wa mikataba mikubwa ya ujenzi wa bandari za uvuvi, bandari za mafuta na gesi, bandari za mizigo, kiwanda cha kuchakata samaki, Chuo Kikuu cha Uvuvi, chelezo na kadhalika haya ni mapinduzi makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kabisa miradi hii itakapokuwa imekamilika kwa wakati, basi itaiondosha Zanzibar na kupiga hatua kubwa sana ya kimaendeleo na changamoto ya ajira kwa vijana ikiwemo vijana wa Jimbo langu la Kikwajuni itakuwa limepata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Magufuli, maono yake haya hayakuwa yameanzia juu juu, mtakumbuka mara nyingi zinapokuja shughuli za uchumi wa bluu miaka ya nyuma alikuwa aki-delegate kwa Rais wa Zanzibar aliyekuwa wakati huo Dkt. Shein, lakini kana kwamba hiyo haitoshi, ameamua kugawa meli nusu kwa nusu bila kujali ukubwa wa kijiografia wala kidemografia kwa Taifa hili kati ya Zanzibar na Bara hii inadhihirisha ni mapenzi makubwa ambayo anayo kwa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge katika hili wameunga mkono naamini hii inadhihirisha umma kwamba muungano wetu huu si muungano wa vitu ni Muungano wa kidugu wa damu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja katika mpango, langu ni moja kwamba juu ya mafanikio yote ambayo tumeyazungumza ni ukweli usiofichika kwamba tuna changamoto ya idadi ya maskini wengi katika nchi hii. Wataalam wanasema kwamba wananchi wa Tanzania ambao wanaishi chini ya Dola 1.9 ni zaidi ya nusu. Ni kweli kasi ya umaskini imepungua kwa mujibu wa takwimu za miaka kumi mpaka 2018, wanasema kasi ya umaskini imeshuka kutoka asilimia 34.4 kuja asilimia 26.4. Hata hivyo, takwimu hizo hizo za wakati huo huo zinaonesha kwamba idadi ya umaskini imeongezeka zaidi ya milioni moja, kutoka maskini milioni 14 kuja 15.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa kuna jambo la kufanya ambapo tunaenda nao, kwanza lazima tujue tatizo ni nini? Tatizo ni moja kubwa la msingi kwamba sekta hizi ambazo zinaajiri watu wengi, kwa zaidi asilimia 66.6 ikiwemo kilimo, mifugo na uvuvi ukuaji wake ni mdogo kulinganisha na sekta ambazo haziajiri watu wengi kama vile ujenzi, huduma, madini na kadhalika. Kwa hiyo kuna haja ya msingi ya kuhakikisha kwamba sasa kipaumbele chetu tunawekeza katika sekta hizi ambazo zinaajiri watu wengi zaidi na kuzifungamanisha sekta hizi na viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kauli mbiu ya mpango wetu wa mwaka ujao unazungumzia kwamba ukuaji wa kujenga uchumi wa viwanda na kuchochea mageuzi ya uchumi na maendeleo ya watu. Sina shaka kwenye maendeleo ya watu tumefanya kazi nzuri, tunapozungumzia kupungua kwa umaskini ni kwa sababu ya kazi nzuri ambayo imefanya kwenye kuwekeza katika sekta ya elimu, katika sekta ya maji, sekta ya umeme vijijini na maeneo mengi, ina maana umaskini umepungua kasi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitajika sasa hivi tuwekeze katika kuona jinsi gani tunaibua fursa za kiuchumi kwa watu ambao wanashiriki katika sekta hizi na njia peke ya kufanya hivyo ni kuona kwamba sasa tunaifungamanisha na viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni yangu ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, nataka tufanye marekebisho katika hii kauli mbiu, badala ya kusema kujenga uchumi wa viwanda ili kuchochea mageuzi ya kiuchumi na maendeleo ya watu mimi nasema iwe na kupunguza idadi ya maskini huku mwisho imalizie hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, bahati mbaya au bahati nzuri jimbo langu mimi sisi tunalima asmini tu, kwa hiyo naomba nitoe mapendekezo zaidi nikijikita katika uvuvi. Jambo la kwanza na kubwa kuliko yote ili viwanda vya uvuvi viweze kusimama lazima wawepo samaki wa kutosha na samaki wa kutosha hatuwezi kuwapata kama hatuna utaratibu mzuri, aidha, wa kupitia public ama private sectors. Kwa hiyo, lazima ili hoja ya Mheshimiwa Rais aliyoizungumza ya kununua meli katika Bunge hili kuanzia bajeti ya mwaka huu tuhakikishe kwamba Serikali tunaishauri inaongeza bajeti ya kuweza kununua angalau meli mbili kila mwaka za uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wewe ni champion wa hili jambo, ulifanya kazi nzuri sana ya kuhakikisha kwamba tunasimamia kupitisha Sheria mpya ya Uvuvi wa Bahari Kuu. Hoja ya uvuvi ya bahari kuu haiepukiki na hoja hii ilipofikia imefikia pazuri, nimpongeze Waziri wa Mifugo na timu yake wameanza kazi vizuri. Sasa hivi kanuni lazima aziharakishe, lazima ahakikishe kwamba wanashirikiana na mwenzake Waziri wa Zanzibar kuharakisha kanuni. Kanuni hizi zitakapokamilika ndipo changamoto nyingi ambazo zilikuwa zikikwaza sekta ya uvuvi na viwanda vitakapokuwa vikipata ufumbuzi ikiwemo suala la tozo na suala la leseni, utaratibu wa exemption na mambo mengine mengi, utaratibu wa kujengea uwezo vijana wetu ili waweze kushiriki katika sekta hii ni na mambo mengi ambayo tuliyajadili vizuri mwaka uliopita kwenye mabadiliko la sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, katika Mpango huu limezungumzwa suala la ujenzi wa Bandari ya Mbegani, kwa mtazamo wangu kwanza bandari moja haitoshi. Nakumbuka Mheshimiwa Rais wa hapa wakati anazindua Bunge alishangazwa sana kuona kwamba ukanda mzima wa bahari hindi kuanzia Lindi, Mtwara, Mafia, Dar es Salaam, Pwani, Tanga, Pemba, Ugunja, hakuna hata kiwanda kimoja cha kuchakata samaki. Hii inasababishwa na nini? Kwa sababu tutakapokuwa tumeimarisha miundombinu mizuri, miundombinu ya viwanda, miundombinu ya bandari na tukaweza kuwajengea uwezo wananchi wakashiriki vizuri katika uchumi huu wa bahari kuu, itasaidia sana kuweza kuchochea sekta hii na sekta ya uvuvi itaimarika na hatimaye tutaweza kupambana na changamoto ya kupunguza umaskini katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nilidharimia kuchangia katika eneo hilo la uvuvi, nakushuru sana kwa kunipa fursa hii. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na afya, lakini nitumie fursa hii kwa mara nyingine tena Mheshimiwa mama Samia Suluhu Hassan kwa imani yake kwangu kwa kunichagua kuwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijikite katika hoja kama mbili ambazo WaheshimiwaWabunge wamezizungumzia katika Bunge lako Tukufu kwenye mchango wa mjadala wa Mpango.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ambalo ninataka kulizungumzia ni kuhusu maoni ya baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kuhusu jinsi gani ambavyo kasi ya ukuaji wa uchumi wetu haiakisi hali halisi ya maisha ya wnanachi wa nchi hii.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa utangulizi kwa kunukuu equation moja ya uchumi ambayo inasema Y=C+I+G+X-M. Ukiangalia equation hii inaweza ikatoa tafsiri nyingi lakini kwa haraka haraka na kwa sababu ya muda nimezichukua kama tafsiri tatu. Ta kwanza inaonesha kwamba kipato na matumizi ni vitu ambavyo vinakwenda sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano leo hii mtu ambaye anafanya biashara anashindwa kupata sehemu nzuri ya kuweka biashara zake na mtu ambaye anaishi katika mazingira duni akiweza kupata uwezo wa kujenga nyumba bora, akiweza kupata uwezo labda wa kukodi sehemu nzuri ya kufanya biashara zake zikawa rasmi zaidi, maana yake ni nini; maana yake ni kwamba ameweza kuboresha maisha yake na hivyo basi kipato chake kimeongezeka.

Mheshimiwa Spika, leo hii tafsiri nyingine ambayo tunaweza tukaiona moja kwa moja hapa ni kwamba uwekezaji wetu katika nchi hii unakwenda sambamba pamoja na kipato chetu. Sekta hii ya uwekezaji na kipato huwa ni muhimu katika msingi wa kuongeza kipato. Ni jambo ambalo haliepukiki na ndiyo maana leo hii tukiangalia sekta ambazo zinaajiri watu wengi kabisa ni kwenye uwekezaji. Hivyo basi, itasaidia kuweza kufanya viwanda vyetu vihamasike, hasa viwanda vile ambavyo vinatumia rasilimali za kilimo, mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Spika, tafsiri nyingine ya mwisho ambayo nimeipata katika equation hii ni kwamba mwelekeo wa matumizi ya Serikali yanachangia vilevile kipato cha wnanachi. Kwa mfano leo Serikali ikiamua kuwekeza katika umeme vijijini au katika miradi ya maji wakandarasi wa ndani wanapata uwezo na wanaweza kuajiri watu wengine na fedha inazunguka.

Mheshimiwa Spika, hoja ya msingi ambayo iko Mezani ni kwamba je, ni kwa kiasi gani mpango wetu huu wa miaka mitano umeweza kuzingatia tafsiri hizi tatu. Wakati huohuo tukiendelea kuhakikisha kwamba tunadhibiti mfumuko wetu wa bei, lakini wakati huohuo tunaendelea kudhibiti fedha haramu isiweze kuzunguka katika uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia mpango wetu una maeneo makubwa matano. Eneo la kwanza linazungumzia kuhusu kuchochea uchumi shindani na shirikishi. Lingine linazungumzia kuimarisha uzalishaji viwandani, kukuza biashara na uwekezaji, kuchochea maendeleo ya watu pamoja na kuendeleza rasilimali watu. Maeneo haya matano ukiangalia kimsingi na ukiangalia nafasi ya sekta binafsi katika kushiriki katika kufanikisha malengo haya ni jambo ambalo haliepukiki. Iwe sekta binafsi kupitia uwekezaji wa ndani, iwe sekta binagfsi kupitia uwekezaji wa nje ambao watatuletea Foreign Direct Investment, iwe uwekezaji wa ubia katika sekta binafsi na sekta ya Umma.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nitumie fursa hii sasa kueleza kwa kifupi kwamba ni kwa vipi Mpango wetu wa Miaka Mitano tumejikita katika kuhakikisha kwamba tunaisaidia sekta binafsi ili iweze kushiriki kikamilifu katika uchumi wa nchi hii pamoja na kuhakikisha kwamba inasaidia kuongeza mzunguko wa fedha katika jamii.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ambalo ni la msingi ni kwamba tutahakikisha tunafanya maboresho ya kisera, kisheria, kitaasisi na kimfumo pale itakapohitajika ili kuondoa vikwazo na kuvutia uwekezaji ikiwemo kwenye masuala ya kodi ili kuimarisha weledi na ufanisi katika kukusanya kodi na kudhibiti ukwepaji kodi bila kutumia mabavu yasiyostahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili; tutaendelea kupanua wigo wa vyanzo vya kodi na wigo wa walipa kodi. Sasa hivi nchi yetu ambayo ina takribani watu milioni 55 ukiangalia tax base yake ya watu wenye TIN Number hawazidi watu milioni nne. Kwa hiyo, jambo hili ni jambo ambalo ni la msingi kabisa kuliangalia katika miaka mitano ambayo tunakuja.

Mheshimiwa Spika, tutahakikisha tunakamilisha miradi yote ya kimkakati ikiwemo mradi wa umeme kama alivyozungumza Mheshimiwa Waziri wa Nishati akiwa anamalizia hoja yake kwa Mwalimu Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo amezungumza Mheshimiwa Waziri wa Nishati, kwamba suluhisho la kuweza kuhakikisha kwamba tunapata umeme wa uhakika na umeme wa bei nafuu ili viwanda vyetu viweze kupunguza gharama ya uzalishaji, ni kwa kutumia vyanzo mchanganyiko. Kwa hiyo, vyanzo vyote ambavyo vimeainishwa katika mpango huu, ikiwemo vyanzo vya makaa ya mawe, vyanzo vya gesi, vyanzo vya hydro na kadhalika, vitatumika.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kujenga mazingira wezeshi kwa wajasiriamali wadogo, wa kati na wakubwa ili waweze kurasimisha biashara zao na kukuza mitaji yao, uwezo wao, ujuzi wao pamoja na uzoefu wao.

Mheshimiwa Spika, jambo la tano ni kuongeza matumizi ya maarifa na ujuzi wa teknolojia madhubuti katika sekta ikiwemo sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi na shughuli mbalimbali zinazojihusisha na usindikaji wa bidhaa nchini ili kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja.

Mheshimiwa Spika, tutahakikisha kwamba tunajenga mazingira mazuri kwa sekta binafsi kuendelea kuendesha shughuli za uzalishaji na uuzaji nje wa bidhaa za kilimo, mifugo na uvuvi zilizochakatwa.

Mheshimiwa Spika, mikakati hii yote ambayo nimeieleza ambayo iko kwenye mpango huu…

SPIKA: Ahsante sana. Malizia kwa dakika moja.

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: …wa miaka mitano inahakikisha kama nilivyozungumza, kuhakikisha kwamba uchumi wetu unakua, nchi yetu inapiga hatua kimaendeleo lakini wakati huohuo tunaimarisha upatikanaji na mzunguko wa fedha katika jamii yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia hii nafasi ili niweze kuchangia kuhusiana na Mwongozo wa Mapendekezo ya Mpango. Naomba nianze mchango wangu kwa kugusia eneo la kilimo ambapo Waheshimiwa Wabunge takribani wengi sana walilizungumza kwa hisia kali, ukiwemo na mwenyewe na msisitizo wako katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kukiri juu ya umuhimu ambao Waheshimiwa Wabunge wameuonesha wa kulitilia mkazo suala la kilimo zaidi katika Mpango wetu. Kwa hiyo, kama Serikali tumelichukua jambo hili kwa uzito wa aina yake na kwa kuwa, huu ni mwongozo basi niwaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba, pale ambapo Mpango utakapowasilishwa utakuwa umetilia maanani eneo hilo kwa uzito ambao unastahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati njema sana tumekuwa tukifanya kazi kwa karibu sana na Wizara ya Kilimo. Tutashirikiana nao wenzetu vizuri kabisa kupanga mpango wetu mzuri, vizuri zaidi katika eneo hili kwa kuzingatia maeneo yote. Msingi wake ni kuhakikisha kwamba, kilimo chetu kinakuwa kilimo cha biashara, kwa maana gani? Kwa maana kwamba, kwa eneo moja ambalo litasaidia katika kuhakikisha kwamba, tunajitosheleza kwa chakula chetu wenyewe hapa nchini, lakini vilevile kwa kuweka mazingira mazuri ya kuweza kusafirisha chakula hiki nje ili iweze kusaidia kuipatia nchi yetu fedha za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, maeneo ambayo tunakusudia kuyatilia maanani ni maeneo yote ambayo Waheshimiwa Wabunge mmeyazungumza. Kwa kuyataja machache kutokana na muda, eneo la kwanza ambalo tunadhani ni la msingi sana ni eneo la mbegu. Eneo la mbegu hili tutaliwekea mkakati mzuri katika mapana yake; kwanza kuhakikisha kwamba, tunashirikisha sekta binafsi kwa utaratibu wa PPP, lakini vilevile kwa kujengea uwezo taasisi zetu kwenye eneo la tafiti kwenye RND ili tuweze kuzalisha mbegu bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nalo vilevile ni muhimu na lenyewe tutaliangalia kwa kina ni eneo la umwagiliaji. Waheshimiwa Wabunge wamezungumza jambo hili kwa kina na hivyo tuwahakikishie kwamba, miongoni mwa miradi ya vielelezo wenye mpango wetu ujao hili eneo la umwagiliaji tutalizingatia kwa uzito unaostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo katika eneo ambalo limekuwa na changamoto kubwa sana sasa hivi kutokana na changamoto ya UVIKO na upandaji wa bei za mbolea duniani, imesababisha kupanda kwa bei na hivyo basi, ni lazima kama Taifa tuje na mkakati wa muda mfupi wa kuweza kukabiliana na tatizo hili, lakini tuwe na muda wa kati na muda mrefu wa kudhibiti tatizo kama hili lisijitokeze tena. Maeneo ni mengi ambayo tutayazingatia kama ambavyo Waheshimiwa wameyazungumza. Kutokana na muda Waheshimiwa Wabunge naomba nisiyachambue, ikiwemo masuala ya masoko, TEHAMA, ugani na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hata katika eneo hili ambalo Waheshimiwa Wabunge wamelizungumza kwa kina sana ikiwemo jinsi gani Benki yetu ya TADB inavyoweza kusaidia katika eneo hili. Nataka niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge, maelekezo ambayo Mheshimiwa Rais aliyatoa na wengi wameyazungumza kwa uchungu kuhusiana na riba; niwahakikishie kwamba, mchakato huu hasa katika eneo la kilimo kuhakikisha kwamba riba zinashuka chini ya asilimia 10, ni mkakati ambao umeshaanza na BOT kwa kutoa maeneo kama matano ya kuzingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa tayari maombi yameshapelekwa na benki kadhaa kwa ajili ya kutumia fursa hii ili riba ziweze kushuka. Bado hatujafikia katika hatua ya kusema kama BOT imeshindwa au haijashindwa. Naomba Wabunge waipe muda Serikali, tutaisimamia BOT kuhakikisha kwamba, hizi benki ama taasisi zilizoomba zihakikishe kwamba, zinatumia fursa hiyo na kutumia fursa ya kushusha riba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi benki ambazo ni za Serikali ikiwemo TADB na benki nyingine zote, hizi tunataka ziwe ndio mfano wa kwanza wa kuhakikisha kwamba zinatekeleza maelekezo ya Serikali. Kwa hiyo, tutazisimamia, kama kuanza kupunguza riba basi ziwe zinaanza hizi benki zetu za Serikali ikiwemo Benki ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka nilizungumzie ni eneo la mikopo. Kwenye hili eneo la mikopo wako Waheshimiwa Wabunge ambao walikuwa wana mashaka kwamba, pengine mikopo hii tunakopa sana; ni kweli, ni sahihi kabisa. Katika miaka ya karibuni tumekopa kwa kiwango kikubwa sana, hilo sio jambo ambalo ni la siri, ni jambo ambalo lipo dhahiri. Kukopa maana yake nini? Maana yake dhana nzima ya kukopa pale ambapo inakuwa matumizi na mapato hayaendi sambamba. Kwa maana kwamba, mna matumizi, mna mapato halafu mna gap katikati ambayo inahitajika izibwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mnahitaji kufadhili miradi mingi sana mikubwa ya maendeleo ambayo itakuwa na tija katika nchi, lakini pengine mapato yakishapatikana hayakidhi kufadhili ile miradi na hili jambo sio geni kwa duniani. Nchi zote duniani zinafanya hivyo ikiwemo hata hizo nchi ambazo zimeendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nini ambacho tunafanya? Tunachokifanya kwanza ni kuhakikisha kwamba, katika eneo hili la mapato ama revenues tunafanya utaratibu wa kuwa na mikakati ya kuongeza mapato yetu kama nchi. La pili, tufanye jitihada za kupunguza matumizi ili ile gape iweze kupungua na hii hofu ya mikopo na yenyewe vilevile iweze kupungua miongoni mwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hili eneo la kuongeza mapato kuna hatua nyingi ambazo tumezichukua na tunaendelea kuzichukua kama nchi, lakini kwa harakaharaka naomba nitaje chache: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa katika chombo kikubwa ambacho tunakitegemea katika kuhakikisha kwamba kinakusanya mapato ni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). TRA kuna hatua ambazo tayari wamezichukua kuhakikisha kwamba, tunakusanya mapato mengi zaidi kwa wakati mmoja kulingana na changamoto zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja katika mambo ambayo Mamlaka ya Mapato inafanya ni kuhakikisha kwamba, tunaongeza vyanzo vipya vya mapato na mapato haya yako ya aina nyingi, kuna mapato ambayo yanatokana na walipakodi wakubwa. Niyapongeze sana maoni ya Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia suala la kufanya utafiti kwenye eneo hili la mawasiliano, mashirika ya sim una kadhalika. Tumepokea haya mapendekezo na tutashirikiana na Wizara husika ili tuliangalie. Tunaamini kwamba, eneo hili litatusaidia kuweza kupata vyanzo vikubwa vya mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwenye eneo la mitandao. Kuna hoja nyingi zimezungumzwa jinsi gani tutakusanya kodi kwenye hizi huduma za mitandao. Hili lenyewe nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, tayari linafanyiwa kazi na Mamlaka ya Mapato Tanzania, lakini na hizi jitihada ambazo Serikali imekuwa ikichukua za kuhakikisha kwamba, tunafungua fursa zaidi za uwekezaji nchini ili sekta binafsi iweze kuingia na tupate wawekezaji wakubwa, zitasaidia kuongeza katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la informal sectors; hawa watu ambao wanaitwa wafanyabiashara wadogowadogo. Tuna mikakati thabiti na juzi mmeshuhudia Mheshimiwa Rais ametoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa soko pale Kariakoo na maeneo mengine mengi. Haya ni mambo ambayo tunafanya kama Serikali ili wale ambao wanaitwa wafanyabiashara wadogowadogo waweze kuku ana walipe kodi. Mambo mengine ni masuala ya mifumo, masuala mengi ambayo tunafanya ya kuhakikisha kwamba, TRA inafanya kazi yake vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vyanzo vingine, mikakati ya kutafuta vyanzo mbadala vya mapato na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende harakaharaka kwa sababu ya muda, kwenye eneo lingine hili la kupunguza matumizi. Tutakapokuwa tuna njia za kuweza kupunguza matumizi kwa maana gani? Kwa maana ya kuhakikisha kwamba, mikopo ambayo tunakopa inakuwa sio mikopo ya kibiashara mpaka pale inapobidi. Kwa hiyo, kwanza tuzingatie sheria; tuna sheria kama tatu ambazo tunazisimamia, Sheria hii ya Mikopo, Dhamana na Misaada, Sura Namba 134, lakini pia kuna sheria nyingine mbalimbali ambazo zinatuongoza jinsi ya kukopa mikopo ya kibiashara ambayo itakwenda kuwekeza katika miradi ambayo inaleta impact kwenye uchumi wa nchi yetu, hilo ni la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vipimo ambavyo vimewekwa vya kisheria kabisa vya kupima mikopo hiyo inakopwa vipi. Moja, ni kwa mfano kuangalia ratio kati ya thamani ya deni la sasa na GDP na nyingine kuangalia thamani ya sasa ya deni na export. Hayo maeneo mawili ni muhimu sana na ndio maana niungane sana na Mheshimiwa Waziri wa Nishati alivyozungumza, miradi kwa mfano ya reli (SGR), miradi hii ya umeme, hii itasaidia sana kuhakikisha kwamba, GDP yetu kama Taifa inakuwa, lakini vilevile na usafirishaji utasaidia kufanya tuweze kusafirisha nje bidhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo maana yake nini? Maana yake uhimilivu wetu kama Taifa utaongezeka. Kwa hiyo, miradi hii ya uwekezaji niwahakikishie kwamba, imezingatia sheria, lakini imeangalia miradi ambayo italeta tija kwa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ya msingi ni kuona kwamba, sasa tunaweza kufanya jitihada na hii ndio kazi ambayo Mheshimiwa Rais Samia ameifanya kwa weledi mkubwa sana, kwamba, lazima tuweze kupata kuimarisha mahusiano yetu na taasisi za kimataifa ambazo zinatoa mikopo ya riba nafuu. Mikopo hii ni muhimu sana, juzi mmeshuhudia 1.3 trillion iliyotolewa jinsi ambavyo imeleta impact kubwa sana katika nchi yetu, imeenda kuchochea shughuli za uchumi kila mahali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba hatuhangaiki kutafuta fedha zenye gharama kubwa, masharti makubwa au riba kubwa kwa ajili ya kufanya miradi, bali miradi hiyo sasa inafanywa kwa fedha ambazo masharti yake ni nafuu mno. Kwa hiyo katika eneo la kupunguza matumizi hata kama itakapofika mahali tunahitaji tulipe deni kwa mwezi, maana yake tukilipa deni ambalo lina grace period ndefu, deni ambalo riba yake ni ndogo, mzigo kwa Serikali unapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la kupunguza matumizi hata kama itakapofika mahali tunahitaji tulipe deni kwa mwezi, maana yake tukilipa deni ambalo lina grace
period ndefu deni ambalo riba yake ni ndogo. Kwa hiyo, mzigo kwa Serikali unakuwa unapungua.

Mheshimiwa Spika, hoja ya msingi na muhimu ni kuhakikisha kwamba fedha hizi zinatumika inavyostahili na hivyo basi ile hoja ambayo Waheshimiwa Wabunge wamezungumza ni hoja ya msingi sana hoja ya kuhakikisha kwamba suala la tuliangalie kama Serikali eneo ambalo lina mapungufu na tunakiri kwamba eneo hili lina mapungufu eneo la kuangalia kuhusu eneo la sera la M & E ufuatiliaji na uthamini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tukiandaa tukijipanga katika kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo hilo kuna jitihada ambazo Serikali imefanya katika kuboresha ufuatiliaji na utathmini wa miradi ya maendeleo kwenye kuandaa hiyo sera ya Taifa ufuatiliaji wa tathmini, kwa kufanya mambo kadhaa. Moja ni kuandaa mfumo wa kitaifa wa kusimamia miradi ya maendeleo ambapo kimsingi utawezesha upatikanaji wa taarifa za miradi kuanzia uibuaji hadi utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jingine ambalo tunafanya ni kuandaa mwongozo wa ufuatiliaji wa tathmini ya miradi na program za maendeleo. Lakini kama kumbe hiyo haitoshi Waheshimiwa Wabunge walipendekeza juu ya umuhimu wa kuishirikisha sekretarieti za mikoa. Ni pendekezo zuri Waheshimiwa Wabunge pendekezo hilo tumelichukua na tutalizingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi maeneo ambayo nilikuwa nimejipanga kuchangia ni hayo nashukuru sana kwa hii fursa.
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Mkataba wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika wa Kuzuia na Kupambana na Ugaidi ya Mwaka 2004
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kwanza kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliopata nafasi ya kuchangia mjadala huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuru na kuipongeza sana Kamati yetu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama inayoongozwa na Mheshimiwa Vita Kawawa kwanza kwa jinsi ambavyo wanatupa ushirikiano na hata katika hoja iliyoko mezani. Mchango wao ulitusaidia sana, na leo hii hali kadhalika maoni na mapendekezo yao; nimuhakikishie Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kamati kwa ujumla kwamba yote ambayo wameyawasilisha tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikianza kuwashukuru waliochangia wote nianze na wewe Mwenyekiti kwa kuwasilisha mchango mzuri kwa niaba ya Kamati na wachangiaji wengine ambao walipata fursa ya kuchangia, ambao ni Mheshimiwa Chumi, Mheshimiwa Seleman Zedi, Mheshimiwa Ighondo, Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mheshimiwa Zahor, Mheshimiwa Ally Kassinge, Mheshimiwa Nollo pamoja na Mheshimiwa Tadayo. Pia nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Jumanne Sagini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla maoni ya wachangiaji kwa asilimia kubwa sana au kwa asilimia zote niseme yanaonekana kuunga mkono Azimio hili ama Itifaki hii. Tunashukuru sana kwa kuunga mkono Azimio hili, lakini tunashukuru kwa kuweza kusaidia kuongezea kuelezea faida nyingi zaidi, ambazo kama taifa tutapata kwa kuridhia Itifaki hii, tunawashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kabisa kwa maelezo hayo na kwa maoni ya wachangiaji sitakuwa na mengi ya kuzungumza hapa leo kwa sababu mengi yaliyozungumzwa yanaenda sambamba na malengo na matarajio ya uwasilishwaji wa hoja yetu. Hata hivyo kuna mambo machache ambayo niliomba nitumie nafasi hii kuweza kuyapatia ufafanuzi kwa kifupi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza ambayo ningeomba nichangie ni hoja ambayo iliwasilishwa na Mheshimiwa Sophia Mwakagenda. Mheshimiwa Sophia Mwakagenda alihoji juu ya kwa nini tumechukua muda mwingi sana tangu Itifaki hii ilivyopitishwa na kusainiwa na kuweza kuwasilishwa leo hapa Bungeni kwa ajili ya kuridhiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, na nitajibu suala hili nikichanganya na hoja ya Mheshimiwa Nollo ambaye alitoa juu ya umuhimu wa kutofanya mambo kwa kufuata matakwa ya mataifa mengine ya nje, ambayo wakati mwingine hutumia changamoto ya ugaidi kwa maslahi binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba taifa letu kama nchi tunafanya vitu kwa umakini mkubwa. Na kama ambavyo mnafahamu ilibidi tuangalie mambo mengi na tutafatakari kama taifa kabla ya kuwasilisha hapa Bungeni juu ya wakati gani ni mwafaka kuiwasilisha hatua hii. Na hiyo inadhihirisha juu ya uhuru wa taifa letu wa kuamua mambo yake yenyewe, kwamba hatufanyi mambo kwa kushinikiza. Pale ambapo tumeona sasa ni wakati ni muafaka kulingana na mazingira ya sasa hivi; na bahati nzuri Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza kwamba ni kweli taifa letu halijakumbana na changamoto za kigaidi, lakini tumeshuhudia viashiria mbalimbali vya kigaidi vikitokeza katika nchi hii katika nyakati kadhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata majirani zetu na wenyewe wamekumbana na matatizo ya kigaidi, na mfano mzuri ni hivi karibuni nilieleza hapa katika hotuba kwamba tulifanikiwa kuweza kuwapeleka watuhumiwa wawili wa kigaidi kutokana na tukio lililotokea Uganda. Hii inaashiria kwamba umuhimu wa Itifaki hii iko moja katika madhumuni yake makubwa ni kusaidia kubadilishana taarifa, kubadilishana uzoefu, kubadilishana mafunzo na ujuzi mbalimbali. Na pengine Itifaki hii itasaidia sana sasa kuweza kurahisisha ubadilishanaji wa taarifa na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Sophia pia alizungumzia juu ya dhana nzima ya matumizi mabaya ya hoja hii ya ugaidi. Nataka nifafanue kwamba Tanzania tuna bahati kwa sababu tumekuwa ni nchi ambayo imejengeka katika misingi ya amani. Na kama ambavyo walizungumza, nadhani Mheshimiwa Zahor, kwamba vitu hivi havijaja kibahati mbaya. Kuna mambo mengi ambayo yamesaidia nchi yetu kuwa katika hali hii ya amani ambayo imekuwa ni mfano wa kuigwa Barani Afrika na duniani kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini moja ya sababu ambayo imechangia kufanya taifa hili liendelee kuwa na amani, ni kwamba misingi ya nchi yetu tangu imeanzishwa tumekuwa makini kudhibiti visingizio ambavyo vinatumika na baadhi ya nchi au baadhi watu katika nchi mbalimbali kufanya vitendo vya kigaidi. Nchi yetu visingizio hivyo tumevidhibiti kwa kiwango kikubwa na jambo hilo limefanyika kutokana na kazi kubwa iliyofanywa na vyombo vyetu vya usalama, lakini kubwa zaidi na waasisi wa taifa hili ambao walipata fursa ya kuongoza nchi hii katika miaka ya nyuma, vilevile pamoja na nchi hii kuweza kuwa katika mikono salama ya chama kilichopo madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, misingi hiyo imesaidia sana kuvifanya visingizio vya kigaidi ambavyo vimekuwa vikitumika, aidha visingizio vinavyotokana na sababu za kikanda, visingizio vya kikabila, iwe visingizio vya kidini visipatikane katika nchi hii kutoka na uongozi dhabiti na imara ambao nimeeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilitaka nilichangie, ni kwamba labda pengine Itifaki hii inaweza ikachangia matumizi mabaya yenye uhalifu wa kigaidi. Kwamba mtu anaweza tu akasingiziwa kwa sababu tu ya kutoa maoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uhuru wa kutoa maoni upo kwenye Katiba, lakini kwenye Katiba hiyo hiyo uhuru huu umewekewa; maana katiba inasema bila kuathiri sheria za nchi; kwa hiyo uhuru huu umewekewa mipaka ya kikatiba. Uhuru wako unaishia pale uhuru wa mwingine unapoanzia. Na sheria za kudhibiti hizi ambazo zimeelezwa zipo sheria nyingi. Kwa mfano kuna Sheria ya Mtandao ambayo inatumika kuweza kudhibiti matumizi mabaya ya uhuru. kwa mfano leo hii huwezi ukasema una uhuru ukaanza kusambaza picha za ngono hovyo hovyo kwenye mitandao ya kijamii au ukazusha tu taarifa za uongo za kudhalilisha watu wengine, au ukazusha taarifa za kuchochea ubaguzi aidha wa kikabila, wa rangi au mwingineo na tukakaa tuseme tu kwamba huo ni uhuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimtoe wasiwasi kwamba tunazo sheria ambazo zinadhibiti mipaka ya uhuru. Hatuwezi kutumia sheria ya ugaidi ama Itifaki hii kudhibiti uhuru wa watu, lakini uhuru wa watu utadhibitiwa pale ambapo utavuka mipaka ya kisheria kulingana na sheria zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la mwisho ambalo nataka nilizungumze ni kuhusu umuhimu wa sheria hii kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengi wameeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi waliochangia, wamezungumzia juu ya umuhimu wa sheria hii katika kuimarisha usalama katika nchi hii. Na usalama wa nchi hii ni jambo ambalo ni muhimu sana katika kusaidia kufanikisha hata kuimarisha uchumi wa nchi yetu. Kuna hoja zimezungumzwa kuhusu jinsi ambavyo taifa letu limepiga hatua kubwa sana hasa katika kipindi cha karibuni katika sekta ya utalii. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Utalii amezungumzia vizuri hilo. Hatuwezi kuendelea kutumia fursa hiyo ya uchumi wa utalii kama amani katika nchi hii haijaendelea kutulia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na matatizo ya kigaidi yamekuwa na athari kubwa sana katika kuteteresha amani ambayo inaathiri si tu utalii peke yake, yanaathiri utalii, uwekezaji, utabiri wa kimasoko (market uncertainty), lakini hata uingiaji wa fedha za kigeni nchini (Foreign Direct Investment). unaathiri vilevile uwezo wa uchumi wa mtu mmoja mmoja, unaongeza umaskini. Kwa hiyo athari za kiuchumi zinazosababishwa na ukosefu wa usalama katika nchi ni nyingi, na ugaidi ni moja ya chanzo kibaya sana cha kuteteresha usalama wa nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia mataifa mengi yakipata athari kubwa za muda mrefu, athari za kupoteza maisha, athari za kusababisha walemavu katika nchi husika, athari za matatizo ya kisaikolojia ambayo yanatokana na matatizo ya kigaidi. Pia athari za uharibifu wa mazingira na uharibifu wa miundombinu. Miji mingi imeharibika ambayo ilikuwa imejengeka vizuri tu kwa miaka mingi sana na kwa nguvu kubwa lakini leo hii imeharibika. Pia machafuko ya ndani na matatizo mengi sana ambayo yanasababishwa na matatizo ya kigaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nichukue fursa hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kuunga mkono Azimio hili. Ni dhahiri kabisa Itifaki hii itakapopitishwa itasaidia sana kama taifa kuweza kujenga mahusiano na ushirikiano katika nchi yetu na mataifa mengine katika kukabiliana na athari za kigaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache naomba sasa nimalizie kwa kutoa hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru. Nianze kwa kuipongeza na kuishukuru sana Kamati yetu ya Mambo Nje, Ulinzi na Usalama chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Vita Kawawa na Wajumbe wote kwa ushirikiano mzuri ambao wanaendelea kutupa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona leo umesoma mabadiliko ya Waheshimiwa Wabunge kwenye Kamati, matarajio yangu Wajumbe wa Kamati hii wataendelea kuomba kubakia hapa kwa sababu tutawa-miss sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie mambo kama matatu mpaka manne kwa harakaharaka. La kwanza ni suala ambalo Waheshimiwa Wabunge, wengi wamelizungumzia kuhusu changamoto ya msongamano wa Wafungwa Magerezani na Mahabusu, ambapo mbali na maoni ya Waheshimiwa Wabunge lakini hata Kamati na yenyewe kwenye taarifa yake ililizungumza hili. Walieleza sababu nyingi ambazo zinaweza kusababisha jambo hili, moja katika mambo ambayo Kamati ilizungumzia ni jinsi ambavyo tuna upungufu wa Magereza nchini lakini wakaeleza vilevile masuala ya kutotumika ipasavyo kwa huduma hizi za Parole pamoja na wategemezi wa adhabu za kifungo kwa maana ya kutokutumia zile adhabu mbadala na nyingine ni hoja ya Wahamiaji haramu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana kabisa na hizi hoja, nitachukua furasa hii kujaribu kueleza hatua ambazo Serikali tumechukua katika kukabiliana na hoja hizi ambazo ni sahihi kabisa. Mbali ya hoja hizi suala la msongamano magerezani ni pana zaidi na upana wake unatokana na hatua ambazo Serikali tumechukua kuliangalia hili, lakini kuangalia kwa ujumla wake utendaji kazi wa Vyombo vyetu vya Usalama kwa ujumla wake na ndipo tukaja na mpango kabambe wa kufanya maboresho makubwa katika vyombo hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapofanya reforms katika jambo lolote changamoto yake ni kwamba, unaweza usipate matokeo haraka, inahitaji ustahimilivu na uvumilivu katika kupata matokeo kwa sababu inahusisha tafiti mbalimbali, inahusisha vilevile marekebisho ya mifumo, marekebisho ya sheria, marekebisho ya mazoea, marekebisho ya aina mbalimbali. Kwa hiyo, naomba nitoe mfano mmoja wa hii kauli yangu ambayo nimeizungumza ya umuhimu wa kuliangalia kwa mapana yake zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama siku mbili nyuma nilipita hapa kwenye Kituo cha Police Central, Dodoma na sikuwa nimemwambia mtu yeyote kama naenda, nilipita tu nikasimama, nikaingia ndani, nikawaambia naomba nizungumze na hawa mahabusu walioko huku ndani. Kwa hiyo nikaingia kwenye mahabusu, nikajaribu kuwauliza hivi kuna mahabusu yeyote hapa anahitaji kueleza jambo lolote kwa Waziri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakajitokeza waliokuwa na hoja zao mbalimbali. Mmoja ambaye nataka nimtolee mfano hapa, aliyejitokeza akalalamika kuonewa na Jeshi la Polisi. Akasema bwana mimi nimekamatwa hapa nimekaa mahabusu muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipofanya utafiti baada ya kuzungumza naye na utafiti mbalimbali kuhusiana na yule mtu, niligundua yule mtu aliwahi kufungwa miaka 30 Ruvuma kwa kosa la ubakaji na alikaa miaka michache gerezani akapata msamaha. Baada ya kupata msamaha, hivi karibuni amekamatwa kwa tuhuma za kubaka watoto wa madrasa, sio mmoja, sio wawili, sio watatu, sio wanne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sio Mahakama, kuna utaratibu wake wa kuweza kutoa hukumu, lakini mazingira ya uchunguzi wangu mimi wa juu juu umenipa imani juu ya umuhimu wa yeye kuendelea kukaa mahabusu. Nina uhakika hata kama ataachiwa leo hivi, pengine akienda huko wanaweza wakamuua wale wazazi wa wale watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nini maana ya kutoa mfano huu? Maana yangu ni kwamba, hata utaratibu huu wa misamaha, utaratibu huu wa parole ambao Waheshimiwa Wabunge wanaulalamikia kwamba tunaufanya kwa kusuasua, na wenyewe unahitaji maboresho na kuangaliwa, kwamba, je, utaratibu tunaoutumia hautoi mianya kwa watu wengine ambao hawastahili kutumia fursa hizi? Kwa hiyo, pengine mambo haya ambayo tunayafanya yanasababisha kuonekana tunachelewa kutumia hizi fursa mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumzwa ni kuhusiana na wahamiaji haramu. Ni kweli, tatizo la wahamiaji haramu ni kubwa sana. Hatua ambazo tunaendanazo mpaka sasa hivi ni nzuri na za kuridhisha, kwa sababu, hivi sasa tunavyozungumza wahamiaji haramu hawa wa Ethiopia waliko gerezani wanakadiriwa kufika 2,673. Katika kipindi cha mwezi Januari na Februari tu peke yake ambapo mwezi Februari ni tarehe za mwanzo tu, tarehe 7, leo tunazungumzia wahamiaji waliorudi kwao Ethiopia kwa miezi hiyo miwili wanakadiriwa kufika 1,538.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipozungumza leo asubuhi nimewasilishiwa release orders za kusaini wahamiaji ambao wako tayari kuondoka 397, hivyo kufanya jumla ya wahamiaji haramu wa Ethiopia 1,903 ambao wanaondoka kwa miezi miwili. Sasa hii ni hatua kubwa sana. Hatua hizi zimesababishwa na nini? Kwanza ni jinsi ambavyo tumelichukulia kwa uzito tatizo hili na kuweza kutoa maamuzi ya muhimu sana. Maamuzi yenyewe ni kuhakikisha kwamba tunaiondoa nchi ya Ethiopia katika nchi ambazo zinatumia utaratibu wa Visa Rejea. Sasa tumefikia katika hatua nzuri kwa sababu tayari tumeshabadilisha kanuni na hivi sasa tunapozungumza tayari GN Namba 37 ya mwaka 2023 imeshatangazwa na hivyo basi, utaratibu wa matumizi ya Visa kwa wananchi wa Ethiopia kuja Tanzania utaendelea kutumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua hii itasaidia sana kwanza kuua hii biashara ya usafarishaji binadamu haramu. Itasaidia pia kufanya Serikali iweze kuongeza mapato kwa sababu, hawa watakuwa wanalipa Visa. Pia itaondoa ile changamoto ya kuiingiza hasara ya Serikali ambayo Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakiipigia kelele. Waheshimiwa Wabunge wa Kamati ya Bunge wamezungumza hapa juu ya takwimu kwamba, pengine kwa kipindi kifupi tu kulingana na takwimu zao tumepoteza karibu shilingi bilioni 5.6, wakashauri wahamiaji hao waondolewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuondoa wahamiaji haramu kwa kutumia gharama za Serikali ni changamoto kubwa. Kwa sababu tulipiga hesabu kwa hawa wahamiaji ambao nimewazungumza, elfu mbili na kitu, kama ingekuwa tumewaondoa kwa fedha ya Serikali, tungetumia takribani Shilingi bilioni tisa, ambapo kama ukijumlisha na hesabu ile ya Waheshimiwa Wabunge madawati, badala ta kupata madawati 31,000 unazungumzia madawati zaidi ya 129,000. Kwa hiyo, ndiyo maana tukatumia njia mbadala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, njia ambazo tumetumia, ya kwanza, tumeweza kuzungumza na washirika wa maendeleo, na wameweza kuondoa wahamiaji haramu zaidi ya 504. Sasa hivi tuna utaratibu mzuri ambapo ndugu wa hawa wahamiaji haramu wenyewe wanakuja sasa kuwaondoa ndugu zao kwa gharama zao wenyewe. Ndiyo maana sasa hivi nazungumzia jitihada hizo kwamba zinakwenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hii hoja ya kuiondoa Ethiopia kwenye utaratibu wa Visa Rejea imeweza kuleta hamasa katika nchi yao kuona kwamba, sasa hivi hakuna sababu tena ya kuweza kutumia njia ya kificho kuweza kusafiri. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninaomba nilizungumzie kwa haraka haraka…

MWENYEKITI: Haya, nakuongeza dakika moja Mheshimiwa umalizie jambo lingine.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja?

MWENYEKITI: Hitimisha ndiyo. Muda wako ulikuwa umeisha Mheshimiwa. Unaweza ukamalizia lakini jambo lako moja ambalo umelisema.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Jambo ambalo nilitaka nilihitimishe kwa haraka haraka ni eneo la Jeshi la Polisi na hasa katika eneo la usalama barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jambo hili kuna mambo makubwa mawili ambayo tunafanya; la kwanza kabisa, ni kufanya reform ambayo juzi nilishuhudia jinsi Mheshimiwa Rais alivyounda tume. Ile tume pamoja na mambo mengine, inakwenda kuangalia mambo mengi; inakwenda kuangalia maslahi, utaratibu wa ajira, na vitu mbalimbali. Pia kuna vitu ambavyo tayari tumeshavianza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema lazima Jeshi la Polisi liwe la kisasa ili tudhibiti uhalifu kwa ufanisi zaidi, ili tudhibiti ajali za barabarani, ili tupunguze kero au malalamiko ya wananchi kuhusu rushwa kwenye Jeshi la Polisi na mengineyo, lazima Jeshi la Polisi liwe la kisasa. Hivyo, kwa upande wa ajali barabarani kwa mfano, kuna mambo makubwa mawili ambayo wakati wowote kuanzia sasa tunaweza kuanzanayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, ni kwamba, tunaanza hivi karibuni kutangaza utaratibu wa kuweza kufanya ukaguzi wa lazima wa magari. Kwa hiyo, naomba kuchukua fursa hii kutoa wito kwa taasisi ama kampuni yoyote duniani ambayo inajihisi inaweza kuja kushirikiana na Serikali. Maana mambo haya yote ya modernization ya Jeshi la Polisi na majeshi mengine, hatuwezi kuyafanya kwa kutegemea bajeti ya Serikali peke yake. Kwa hiyo, kuna utaratibu ambao tunaweza tukashirikisha taasisi binafsi kwa ajili ya kwenda kukabiliananayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni jambo jema kabisa, ni kitu muhimu sana kuweza kuwa na mifumo ambayo itasaidia Jeshi letu la Polisi kuweza kubaini makosa ya uhalifu kwa haraka, ikiwemo makosa ya jinai, makosa ya ajali barabarani na mengineyo. Kwa hiyo, hatuwezi kuepuka katika karne ya leo kuwa na matumizi ya mifumo ya kisasa ya kamera.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuna mpango vilevile katika muda siyo mrefu kuanza utaratibu wa kuwa na mifumo ya miji salama katika nchi hii. Haya mambo niliyazungumza katika bajeti iliyosomwa mwaka uliopita 2021/2022 na katika utekelezaji wake tumefikia katika hatua ya kuridhisha. Tutaanza na Mji wa Dodoma, Mji wa Dar es Salaam, Mji wa Arusha na baadaye tutaelekea na miji mingine mikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna hoja nyingine ya vitendeakazi. Katika hili Mheshimiwa Rais Samia suluhu Hassan amefanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua unataka kunikatisha, lakini angalau moja niliseme la muhimu kwa sababu Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakizungumza sana katika maswali mbalimbali hapa Bungeni wakiuliza Wizara yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba, sasa hivi tunakamilisha utaratibu wa kuweza kupeleka magari katika kila Wilaya katika nchi hii. Kwa hiyo, kila Mbunge ambaye ana changamoto ya gari katika jimbo lake, sasa inaendelea kupatiwa ufumbuzi. Fedha hiyo Mheshimiwa Rais ameshaitoa na wakati wowote magari haya, taratibu za manunuzi zitakapokamilika yataingia na tutaweza kukabiliana na changamoto hiyo ya usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengine ambayo yanahusu masuala ya makazi na vituo vya Polisi…

MWENYEKITI: Ahsante sana Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi.
Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa hii ya kuweza kuchangia. Nianze kukupongeza wewe binafsi kwa kuweza kuchaguliwa kwa kura za kishindo, kuwa Spika wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia nichukue nafasi hii kuishukuru sana Kamati yetu chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Zungu, ambaye na yeye nimpongeze kwa kuweza kupitishwa na Chama chetu kuwa Mgombea wa Naibu Spika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli Kamati hii kwa muda mfupi ambao nimeweza kushirikiana nayo imetupa ushirikiano mzuri sana. Nafarijika sana kuwa ni miongoni mwa Wajumbe wa Kamati hii. Kwa hiyo nawashukuru sana, nawapongeza sana kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kufanya. Hata hivyo, pamoja na taarifa nzuri ambayo imewasilishwa hapa leo, nataka nijikite katika maeneo kama matatu hivi ambayo Kamati iliyazungumzia lakini na baadhi ya Wabunge waliyagusia ni kwa upande wa Jeshi la Magereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja mbili kwenye Jeshi la Magereza. La kwanza, ilikuwa ni jinsi gani Jeshi la Magereza linaweza likajitosheleza na chakula, lakini na la pili, lilikuwa linahusu hoja ya kupunguza msongamano kwenye Magereza yetu. Sasa nasema hoja hizi mbili naweza nikazichangia kwa pamoja kwa sababu zinaingiliana. Kwa nini nasema zinaingiliana? Tunapozungumzia dhana nzima ya Magereza kujitosheleza na chakula ni jambo la msingi sana.

Mheshimiwa Spika, haiingii akilini kabisa kwamba Jeshi la Magereza, ambalo lina rasilimali ardhi yenye rutuba ya kutosha, lakini tunasema ina nguvu kazi pia ya kutosha, iwe inaendelea kutegemea ruzuku ya Serikali katika kuhudumia wafungwa. Imani yangu ni kwamba sio tu kwamba linaweza kujitosheleza na chakula, lakini linaweza likazalisha ziada kwa ajili ya kuweza kulipatia Jeshi la Magereza mapato yatakayosaidia kupunguza changamoto mbalimbali za Jeshi letu. Sasa ninaposema hizi hoja zinaingiliana nina maana gani? Hivi tunavyozungumza mpaka leo tuna takribani watu bilioni 32, ambao kati ya hao kama milioni 18.2 ndio wafungwa, lakini kuna milioni 13.8, hawa ni mahabusu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunapozungumzia suala la wafungwa kuwatumia kama nguvu kazi ya kulima ili tujitosheleze na chakula, kuna changamoto lazima tuje na mawazo na ubunifu mwingine wa ku-address jambo hili. Kwa sababu, hatuwezi tukasema kwamba katika karne hii tunayoendelea wakati hoja ya kutaka kupunguza wafungwa Magerezani inakuwa ina umuhimu wake mkubwa, halafu tuseme tuwa-retain wafungwa hawa kwa sababu, eti tunataka watusaidie kujitosheleza na chakula.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hapa kuna vitu lazima tuvi-address kwa kutumia ubunifu wa hali ya juu. Ndio maana tumeamua sasa hivi kuja na utaratibu ambao nataka niueleze hapa kwa ufupi. Utaratibu huu utasaidia sana kulifanya Jeshi letu la Magereza, liweze kujikita zaidi na lile jukumu lake la msingi la kurekebisha wafungwa. Kumekuwepo na baadhi ya hoja kwa baadhi ya watu wanasema, baadhi ya wafungwa wanaweza wakaachiwa sasa hivi, halafu baada ya muda mfupi wanarudi kuwa wahalifu. Nasema pengine kwa sababu labda, Jeshi la Magereza linajikita sasa katika kufanya mambo mawili kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati huo huo Jeshi la Magereza tunasema lirekebishe wafungwa ambalo ni jukumu lake la msingi, lakini tunasema wakati huo Jeshi la Magereza tunataka lijitosheleze na chakula, liweze kubuni miradi mbalimbali, viwanda na kadhalika. Basi mambo haya tunataka tuyafanye kwa pamoja, lakini kwa utaratibu ambao utatenganisha majukumu yake. Ndio maana tuna mkakati kabambe wa kuhakikisha kwamba mashirika yote ya uzalishaji mali katika Majeshi yetu, ikiwemo Jeshi la Magereza yanasimama na kujiendesha kibiashara. Ili kuliacha Jeshi la Magereza kama Jeshi kufanya kazi zake za msingi za kurekebisha wafungwa na mengineyo yaliyopo kwa mujibu wa Katiba pamoja na Sheria za Nchi yetu na Kanuni zake. Katika kufanya hivyo ni imani yetu kwamba… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde chache malizia.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema kwamba, kuna mambo ambayo kama Serikali yanaendelea kufanyika. Nimpongeze sana Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, katika sherehe za Uhuru hivi karibuni amesamehe wafungwa, zaidi ya 5,704. Hizi ni katika jitihada za kupunguza msongamano magerezani. Kana kwamba hiyo haitoshi, kuna hatua nyingi ambazo tunaendelea, kuzichukua na tunaamini hizi zitasaidia kupunguza msongamano wa wafungwa. Moja, tuna sheria zetu kuna Sheria ya Parole. Kuna Sheria ya…(Makofi)

SPIKA: Sasa, Mheshimiwa Waziri muda umetutupa mkono.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba nichukue fursa hii kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri. Kwa sababu ya muda hatutaweza kutoa ufafanuzi wa michango yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wameiwasilisha, lakini niwaahidi kwamba tutaichukua na tutaifanyia kazi na mengine tutaweza kuwasilisha majibu yake kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, katika michango ya Waheshimiwa Wabunge hasa hasa imejikita katika maeneo makubwa matatu, eneo la kwanza ni kuhusiana na changamoto ya mazingira ya askari wetu ambayo wanafanyia kazi, lakini lingine linahusu mazingira pamoja na vifaa ama zana za kufanyia kazi. Waheshimiwa Wabunge wengi wameonesha kuguswa kwao na jinsi ambavyo askari wetu wa vyombo vyote vya usalama vilivyopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, wanavyoishi katika mazingira ambayo ni duni, vituo vya kufanyia kazi hususani Vituo vya Polisi, Magereza na kadhalika, vikiwa katika hali mbaya na maeneo mengine havipo kabisa. Pia katika masuala yanayohusu vyombo vya usafiri, mitambo mbalimbali ya kisasa ya kufanyia shughuli zao zikawa nyepesi zaidi na mengineyo.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la pili ambalo Waheshimiwa Wabunge wameligusa zaidi ni eneo la weledi wa askari wetu. Kwa hiyo linagusa masuala ya umuhimu wa mafunzo, vifaa vile vile vya kufanyia hayo mafunzo stahiki ya askari wetu na mengineyo ambayo kwa ufupi nitayafafanua baadaye.

Mheshimiwa Spika, lingine la tatu ni suala la uadilifu, ambapo hapa linahusisha mambo mengi ikiwemo suala zima la kuwa na mifumo ambayo inaweza ikasaidia kupunguza ubadhirifu hususani kwenye kukusanya maduhuli, lakini pia katika eneo la enforcement kwenye suala la kusimamia sheria na eneo la mafunzo halikadhalika linaingia hapa. Sasa haya ndio maeneo matatu ambayo nimeona nichukue muda huu wa dakika 10 ulizonipatia kuweza kuyatolea ufafanuzi kwa haraka haraka.

Mheshimiwa Spika, nianze na hili eneo, lakini kabla sijazungumza nataka niwakumbushe suala moja. Nilipokuwa nasoma hotuba leo asubuhi, nilieleza kitu kimoja kikubwa sana na nina hakika Waheshimiwa Wabunge watakikumbuka, nilieleza kwamba Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan mara hii amefanya mapinduzi makubwa ya kibajeti katika vyombo vya usalama vilivyopo Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Nikatoa takwimu kuna ongezeko la fedha nyingi sana. Kwenye fedha za maendeleo zimeongezeka kwa wastani wa zaidi ya Sh.112,942,900,000, lakini katika eneo linalohusu matumizi mengineyo na kwenye kuna zaidi ya Sh.80,000,000,000 zimeongezwa kwa mara ya kwanza chini ya utawala wa Mama Samia Suluhu Hassan. Hii ni dhamira yake ya dhati na mapenzi yake aliyokuwa nayo makubwa kwa vyombo vyake vya usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hiyo dhamira ya Mheshimiwa Rais ambayo leo Waheshimiwa Wabunge hapa wakipitisha bajeti hii tunakwenda kuona changamoto hizi walizozungumza kwa kiasi fulani zinaanza kupatiwa ufumbuzi, pamoja na mambo mengine ambayo nilieleza asubuhi yanayohusu ubunifu.

Mheshimiwa Spika, katika suala la mafunzo ambalo lina mchango mkubwa sana katika kuimarisha weledi na uadilifu wa Askari wetu, hili na lenyewe limetendewa haki. Kwa mara ya kwanza katika historia, baada ya muda mrefu, leo hii Askari Polisi kama nilivyozungumza asubuhi, wametengewa bajeti ya zaidi ya shilingi bilioni 16.6 kwa ajili ya kwenda kwenye mafunzo bila ya kukatwa hata senti tano. Hili ni jambo ambalo kwa kweli linahitaji sana kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa kuweza kuwaona Askari wetu na hiki kilio chao cha muda mrefu kuweza kukipatia ufumbuzi. Ni imani yangu sasa hii itasaidia kujenga uwezo wa Askari wetu na kuimarisha vile vile morale ya Askari hawa katika kutekeleza majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika bajeti hii vile vile fedha hizi ambazo mmeziona zimeongezwa zimegusa katika maeneo yanayopelekea kuongeza ukusanyaji wa mapato na kuzuia uvunjifu wa ukusanyaji wa mapato hayo. Kwa mfano, katika maeneo ambayo yametajwa, nampongeza sana Mheshimiwa Deus Sangu, amezungumzia kuhusiana na suala la mfuko wa tuzo na tozo; bahati mbaya kwa sababu ya muda siwezi kueleza.

Mheshimiwa Spika, katika jambo moja ambalo tunachukua hatua ya kibajeti, ni kuhakikisha kwamba sasa tunakuja na mfumo ambao utakuwa ni madhubuti katika kusimamia mfuko wa tuzo na tozo, badala ya utaratibu wa sasa hivi ili kuepusha kukutanisha binadamu ambao mara nyingi inaweza kuchochea mazingira fulani ya rushwa. Kwa hiyo, moja katika jambo ambalo tunafanya katika bajeti hii ni ku-address tatizo la Mheshimiwa Deus Sangu kwenye hilo tatizo la tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine la mifumo katika bajeti hii linakuja kuangaliwa kutokana na kazi nzuri ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, ni eneo la kwenye masuala ya kinga na tahadhari za moto kwenye Jeshi la Magereza. Kumekuwa na kwenyewe kuna mianya fulani ya upoteaji wa fedha katika kutoa elimu na kwenda kufanya ukaguzi. Maeneo haya yameangaliwa na tunakuja sasa na mifumo ambayo itasaidia kupunguza upotevu huo.

Mheshimiwa Spika, mifumo hii siyo tu katika masuala ya maduhuli na kadhalika, lakini hata katika kuimarisha utendaji kazi wa Askari wetu. Leo hii watu wamekuwa wakilalamika kuna msongamano Magerezani, lakini moja katika sababu hiyo ni ucheleweshaji wa upelelezi; na wakati mwingine ucheleweshaji wa upelelezi huo unaweza kuwa unachangiwa na kutokana na vitendea kazi duni.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, leo katika bajeti hii tumeweza kuweka fedha za kuridhisha kwenye kitengo cha Finance cha Jeshi la Polisi ili tuweze kuhakikisha kwamba tunasaidia kuongeza weledi katika kukusanya taarifa za kipelelezi na taarifa hizo ziweze kutumika kwa ufanisi zaidi katika kutoa maamuzi ya wahalifu ama kwenye kesi zinazoendelea Mahakamani.

Mheshimiwa Spika, mambo ni mengi, hata katika mfumo wa kiintelejensia na mengineyo. Naomba niende haraka haraka kwa sababu ya muda, nisije nikaacha na mengine nisiyaguse.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo lilizungumzwa ni hoja ya stahiki za Askari. Ni hoja ya msingi, lakini nataka nitoe mfano mmoja kwa haraka haraka. Katika bajeti hii tuna zaidi ya shilingi bilioni 1.56 ambazo zinatumika kwa ajili ya kulipa wastaafu. Kwa hiyo, utaona kwamba safari hii changamoto ya wastaafu kulipwa stahiki zao inapatiwa ufumbuzi kwa kuongeza fedha ya kiwango kikubwa katika bajeti yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo katika bajeti hii ya Mama (naiita) imefanya hoja za Waheshimiwa Wabunge ziweze kupatiwa ufumbuzi ni kwenye suala zima la kuimarisha mazingira ya makazi ya Askari wetu, mazingira ya vituo vyetu vya Polisi, mazingira ya vifaa vya kufanyia kazi, mazingira ya mitambo, Magereza yetu; yote haya mkiangalia kitabu cha bajeti mtaona kuna hatua kubwa sana imepigwa.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, naomba nirudie kwa haraka haraka kwenye mambo ambayo nadhani tumeyagusa. Nikiangalia kwenye eneo la ujenzi wa Askari, tumekuja na mpango kabambe wa miaka 10 wa kukabiliana na changamoto ya makazi ya Askari. Katika mpango huo ambao utaanza mwaka 2022/2023 mpaka 2031/2032 mpango huo wa miaka 10 tunatarajia kujenga nyumba zaidi ya 51,780 za Askari. Tukifanya hivyo maana yake changamoto ya makazi ya Askari tutakuwa tumeipatia ufumbuzi kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kana kwamba hiyo haitoshi, katika mpango wetu huo tunatarajia kujenga ofisi 44 za Makamanda wa Mikoa; ofisi 12 za Wakuu wa Vikosi; Ofisi 135 kwenye ngazi ya Wilaya; na zahanati na kadhalika. Kwa hiyo, hayo ni mambo ambayo ni makubwa sana, ingawa kuna mambo mengine ambayo tunajaribu kuyafikiria, sikutaka kuyazungumza kwenye bajeti kwa sababu ni masuala ambayo wakati muafaka utakapofika tutayazungumza.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya kuwaonesha Waheshimiwa Wabunge dhamira ya dhati ya Serikali katika kukabiliana na changamoto hizi za makazi, changamoto za vituo vya Polisi na kadhalika, tuna mipango mingine mbadala; na moja katika mpango ambao nataka niudokeze sasa hivi kwa haraka haraka, niliuzungumza katika hotuba asubuhi kwamba tunadhamiria kuimarisha mashirika yetu ya uzalishaji mali ili yaweze kufanya kazi kibiashara.

Mheshimiwa Spika, mashirika haya yaliundwa kwa dhamira ya kusaidia kutatua changamoto za vyombo hivi. Kwa sasa hivi tumekuja kwa mpango madhubuti na mkakati thabiti wa kufanya mashirika haya yajiendeshe kibiashara. Ni imani yangu katika muda siyo mrefu sana, tutaona matunda makubwa ya contribution ya mashirika haya katika kutatua changamoto za Askari ikiwemo za makazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mambo ni mengi ambayo nadhani katika kipindi kijacho tutaona mabadiliko makubwa sana ya vyombo vyetu hivi vya usalama kuanzia ujenzi wa Magereza, vituo vya zimamoto, ofisi za Uhamiaji na kadhalika. Hata magari haya ambayo yamezungumzwa, nina hakika katika bajeti hii tumefanya kwa kadri bajeti inavyoruhusu kwa mfano Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia kuhusu changamoto ya Jeshi la Magereza katika kupeleka mahabusu; ingawa tumetenga fedha katika bajeti hii kwa ajili ya kununua magari 32 ikiwepo magari 10 kupeleka mahabusu.

Mheshimiwa Spika, kwa kupitia mikakati hii ambayo nimeieleza, maana yake sasa tunakwenda kuzungumzia magari ya kutosha kwa Magereza kupeleka mahabusu, tunakwenda kuzungumzia kutatua changamoto nyinginezo ikiwemo na msongamano wa wafungwa Magerezani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili eneo la zana; ninapozungumzia hoja ya msongamano wa wafungwa ambayo imezungumzwa sana na Waheshimiwa Wabunge; moja ya sababu kubwa inachangiwa na hivi vifaa vya kufanyia kazi ama zana za kufanyia kazi ama vitendea kazi ikiwemo Magereza yetu. Kwa hiyo, tuki-address hoja ya ujenzi wa Magereza, lakini wakati huo tuna mikakati mingine ambapo hili nimeona nilizungumze kipekee kwa sababu limeguswa sana na Waheshimiwa Wabunge la msongamano wa wafungwa, kwa hiyo, kuna mikakati mingine ya kipekee ambayo haihusiani na miundombinu peke yake, ni kama Serikali tunavyofanya.

Mheshimiwa Spika, moja katika mikakati hiyo ni kutumia sheria zetu. Tuna sheria kama nne ikiwemo sheria ya EML, ya kifungo cha nje; kuna Sheria ya Parole, kuna Sheria ya Uangalizi, kuna Sheria ya Huduma ya Jamii. Vile vile nataka nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais, amekuwa akitumia mamlaka yake ya kikatiba kupunguza msongamano wa wafungwa kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka uliopita peke yake tumeshuhudia zaidi ya wafungwa 9,730 wakiachiwa huru kupitia msamaha wa Mheshimiwa Rais. Kupitia hizi sheria nne nilizozitaja hapa, kuna wafungwa wengi ambapo kila mwaka wale ambao tutakuwa tumejiridhisha wamerekebika tutaendelea kuwaachia ili kupunguza msongamano wa mahabusu Magerezani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika tunaendelea kufanya utaratibu wa kushirikiana na mamlaka nyingine. Kwa mfano, tuna utaratibu ambao tunashirikiana na Ofisi ya DPP, Ofisi ya TAKUKURU ya kuharakisha ama kuhamasisha ushirikiano kwa kushughulikia mashauri ya kesi jinai. Katika kufanya hivyo, Kamati hii inapita katika Magereza kuweza kupitia na kuangalia uwezekano wa aidha kuwaachia wale mahabusu wanaostahili kuachiwa.

Mheshimiwa Spika, hili jambo ni muhimu kwa sababu tunapozungumzia msongamano wa wafungwa haugusi katika eneo la wafungwa peke yake, sehemu kubwa vile vile ina mchango wa mahabusu. Kwa hiyo, tutaangalia njjia ambazo tutatumia kutatua changamoto ya msongamano wa wafungwa, lakini kwa utaratibu huu tunakwenda kutatua tatizo la msongamano wa mahabusu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hiyo ni miongoni mwa mikakati ambayo tunafanya. Pia katika eneo hili, tunaendelea kufanya mambo makubwa sana katika bajeti hii. Nilizungumza kwamba sasa katika Magereza yetu…

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, dakika tatu, malizia.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kuna hoja nyingine ambayo ilizungumzwa kuhusiana na ajali za barabarani na hususan ajali za bodaboda na hoja ya takwimu. Naomba nikiri kabisa, kama ambavyo hotuba yangu nilivyoisoma asubuhi, imeeleza kwamba kuna ongezeko kidogo la ajali za barabarani, ingawa nilieleza hatua ambazo kama Serikali tumechukua. Tokea hatua hizo tumeanza kuzichukua, tumeona kuna upungufu wa ajali barabarani. Ni imani yangu kwamba tukiendelea kusimamia mikakati ambayo tumeipanga, tutaweza kupunguza kwa kiwango kikubwa ajali za barabarani.

Mheshimiwa Spika, tatizo la vijana wetu wa bodaboda linagusa maeneo mengi na Jeshi la Polisi kupitia Kikosi cha Usalama Barabarani limeendelea kufanya jitihada kubwa za kupambana na ajali za vijana wa bodaboda. Ajali za bodaboda mara nyingi zinachangiwa na vijana hawa kutokufata sheria. Kwa hiyo, kuna hatua za kujaribu kutoa elimu kupitia kwenye vijiwe vyao, kupitia kwenye stendi mbalimbali wanazokaa, kuwaelimisha juu ya umuhimu wa kufuata sheria za barabarani ili kuhakikisha kwamba wanasimamia sheria kwa wale ambao sasa baada ya kupewa elimu bado wanaendelea kukiuka sheria za barabarani.

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi kama ambavyo nimezungumza katika hotuba yangu, ni kwamba sasa chini ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita ya Mama Samia Suluhu Hassan, tunataka kufanya vyombo vyetu vya usalama vifanye kazi kisasa. Hivyo tuna mpango katika bajeti hii ya mwaka 2023 kupitia Bunge lako Tukufu kama ambavyo nimelieleza asubuhi, ni kwamba tuna mpango wa kuweka mifumo ya kisasa ya ufuatiliaji wa uvunjifu wa sheria. Kuna project kwa lugha ya Kiingereza wanaita safercity (Miji salama) ambayo itahusisha uwekaji wa Kamera za barabarani na mitambo ya kisasa ya kubaini uvunjifu wa sheria ikiwemo uvunjifu wa sheria za usalama barabarani.

Mheshimiwa Spika, hayo ni miongoni mwa mambo ambayo tunadhani tukiyafanya kwa pamoja yatasaidia sana kuweza kupunguza ajali za barabarani kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba sasa kutoa hoja.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru wewe kwa dhati kabisa kwa namna ambavyo umeongoza na kusimamia vyema majadiliano haya ya kupitisha Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka 2023/2024.

Pia nichukue fursa hii kuwashukuru kwa dhati kabisa Waheshimiwa Wabunge wote kwa usikivu, kwa uchangiaji wenu makini uliofanywa kwa kuzungumzwa moja kwa moja katika Bunge hili Tukufu pamoja na kwa njia ya maandishi. Naomba niseme kwamba, tunatambua na kuthamini dhamira na nia njema ambayo mnayo ambayo kimsingi inalenga kuboresha mikakati na mbinu za kufanya kazi katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya NUU chini ya Mheshimiwa Mwenyekiti Vita Rashid Kawawa pamoja na Makamu Mwenyekiti, Mheshimiwa Vincent Mbogo na Wajumbe wote kwa jinsi ambavyo walivyoweza kuwasilisha Taarifa ya Kamati iliyosheheni na yenye maelekezo na ushauri mzuri. Nao niwaahidi kwamba ushauri huo tutauchukua na kuufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja za Wabunge ni nyingi na waliochangia ni wengi. Naomba nizijibu hoja hizi, zile ambazo nitaweza kuzijibu sasa hivi kuzifafanua bila kuorodhesha majina tuweze kuzijibu kwa pamoja kutokana na wingi na wengi wake. Nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jinsi ambavyo ameweza kutoa ufafanuzi wa hoja mbalimbali kabla yangu mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwashukuru tena kwa mara nyingine tena Waheshimiwa Wabunge kwanza kwa kuthamini jitihada kubwa sana za Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu. Hii inadhihirisha kwamba Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Rais na Serikali yake tunazungumza lugha moja, tunacheza wimbo mmoja, tunatembea pamoja. Tunashukuru sana kwa kuunga mkono jitihada hizo ambazo Mheshimiwa Rais amekuwa akizifanya toka ameingia madarakani za kuhakikisha kwamba anashughulikia changamoto za Askari na vyombo vya usalama katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Kiongozi Mkuu wa nchi yeye amekuwa ndio mpambanaji namba moja wa kuhakikisha kwamba vyombo hivi vya usalama vinatekeleza majukumu yake katika mazingira mazuri na kwa weledi. Nadhani sisi tunapaswa kufuata nyayo zake. Waheshimiwa Wabunge mmelionesha hilo katika michango yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa jinsi ambavyo wametupongeza na wamependezwa na vyombo hivi vinavyofanya kazi zake vizuri, lakini hawajasita kuonesha maeneo ambayo wanadhani ni vyema yakafanyiwa kazi ili tuweze kuviimarisha vyombo vyetu vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii sasa kuweza kutoa ufafanuzi wa mambo hayo, lakini kabla sijafanya hivyo, kuna hoja moja naomba nianze nayo ambayo nimeona siyo sawa nianze ufafanuzi bila kuizungumzia hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua Waheshimiwa Wabunge wamezungumza kwa uchungu na hasira kutokana na jinsi ambavyo wanaona kuna haja ya kufanya jitihada zaidi za kuweza kuimarisha vyombo na Askari wetu. Katika mazingira yoyote yale, hakuna namna ambavyo tunaweza kuhalalisha rushwa, hakuna namna ambavyo tunaweza kuhalalisha uzembe, hakuna namna ambavyo tunaweza kuhalalisha uonevu, hakuna namna ambavyo tunaweza kuhalalisha kupora haki ya watu kwa kisingizio chochote. Iwe kwa maslahi madogo, iwe kwa kucheleweshwa kwa haki hizo na maslahi hayo. Kwa hiyo, hili naona nilizungumze likae kwenye rekodi na nina hakika Waheshimiwa Wabunge nao pia wanaamini kama ambavyo ninaamini mimi kwamba tuna haja ya kuhakikisha kwamba tunawatendea haki wananchi wa nchi hii kwa kuepuka vitendo vyote ambavyo ni kinyume na maadili na uadilifu kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama. Hilo niliona nilizungumze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanya hivyo, ndiyo maana kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri tutaendelea kuhakikisha tunachukua hatua za kisheria kwa yeyote yule, iwe Askari, iwe mtumishi raia katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ambaye atakiuka maadili mema ya utendaji kazi wake lakini hatutaacha kuwapongeza wale wote ambao wanafanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi ni mashahidi. Leo kuna Askari mmoja mwenye cheo kidogo tu alifanya kitendo cha kishujaa na cha kupigiwa mfano. Tulimleta hapa Waheshimiwa Wabunge mmemwona na tumemtambulisha kwenu na baadaye jioni tukitoka hapa tuna tafrija, yeye pamoja askari wengine waliofanya vizuri kwenye kata, tukiona kwamba ni utaratibu mzuri wa kuweza kutoa motisha kwa Askari wengine; naamini waliofanya vizuri ni wengi, lakini tutaendelea kufanya hivi kila mwaka ili kuweza kutoa motisha kwa Askari wengine ili watambue kwamba tunathamini juhudi za Askari waadilifu, tunathamini juhudi za askari ambao wanafanya kazi zao kwa kujituma na kwa ubunifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zilizozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge kwa uchungu kabisa ni nyingi. Wamezungumzia kwa mfano masuala ya vitendea kazi. Wako waliozungumzia masuala ya usafiri, magari, boti, vitendea kazi vingine mbalimbali kama pikipiki, hata helicopter naongezea hiyo, lakini wako Waheshimiwa Wabunge walizungumzia juu ya changamoto ya vituo vya Polisi katika maeneo yao, nyumba za makazi ya Askari. Kuna masuala ya stahiki na madeni ya muda mrefu ya Askari Polisi, masuala ya mafunzo, masuala ya vitendea kazi vya kisasa, mifumo, TEHAMA, vifaa, zana, sare na kadhalika. Mambo mengi yamezungumzwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba kutokana na dhamira njema ya dhati ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, tokea ameingia madarakani, amefanya kazi kubwa sana ya kuboresha vitendea kazi katika vyombo vyetu vya usalama. Ndiyo maana katika bajeti hii ambayo tunamaliza nayo, ambayo imetekelezwa kwa zaidi ya 80% na ni historia katika Wizara hii kutekeleza bajeti za Mambo ya Ndani kwa zaidi ya 80%, kuna ziada ya zaidi ya Shilingi bilioni 300. Amekuta bajeti ya shilingi bilioni 900 kufikia Shilingi trilioni 1.1 na mwaka huu tumeongezeka kidogo. Kwa hiyo, dhamira ya Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu inadhihirishwa kutokana na namba zilizopo katika bajeti yetu. Namba hazisemi uongo. Kwa hiyo, hili Waheshimiwa Wabunge nataka niwahakikishie kwamba dhamira ya Mheshimiwa Rais tokea ameingia madarakani ni dhamira ya dhati na dhamira ya vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata katika suala la ulipaji wa madeni na stahiki mbalimbali, katika mwaka huu wa fedha, shilingi bilioni 82.52 zimetolewa kwa ajili ya kazi hiyo. Ni fedha nyingi, najua fedha hizi zinaweza zisiwe zimekidhi kuweza kutatua matatizo au changamoto ya miaka mingi sana ya madeni ya Askari na kadhalika, lakini angalau kuna kazi na hatua imepigwa. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, tutaendelea kuhakikisha kwamba tunachukua maoni yenu na kufanya jitihada zinazowezekana kupunguza madeni haya ya askari kwa kadiri ya hali ya kiuchumi itakavyoruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ambalo linadhihirisha juu ya dhamira ya dhati ya Serikali katika kwenda sambamba na dhamira ambayo Waheshimiwa Wabunge wanayo ni kwamba katika kipindi cha mwaka huu tunaomaliza nao, tumeweza kutekeleza miradi 23. Nimekuwepo katika Wizara hii kwa muda mrefu. Ni kwa miaka mingi sana katika kumbukumbu yangu ambapo miradi 23 imekamilika. Miradi hii imekamilika; nazungumza kwa taarifa zilizopatikana mpaka mwezi huu. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kuna miradi kadhaa ambayo inafikiwa katika hatua ya mwisho, kabla ya mwisho wa mwaka huu kumalizika itakuwa imekamilika na hivyo kuongeza hata idadi ya miradi 23 na kuwa miradi mingi zaidi. Miradi hiyo nimeitaja kwa kina katika hotuba yangu, sina haja ya kuirejea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia stahiki za Askari, unazungumzia mambo mengi. Kuna masuala kwa mfano ya upandishwaji vyeo. Kumekuwepo malalamiko ya muda mrefu ya Askari kutokupandishwa cheo lakini katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, watumishi zaidi ya 1,696 wamepandishwa vyeo, lakini mwaka huu ambao tunazungumza nao hali kadhalika tunatarajia kupandisha vyeo askari wengi zaidi. Askari hao ambao wamepandishwa vyeo ni miongoni mwao ni wale Askari ambao tumewapeleka katika kata, wenye vyeo hivi vya ukaguzi na ambao wanaendelea kufanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata katika ajira, tumeweza kutoa ajira kwa watumishi 6,608 katika kipindi hiki, katika mwaka ambao unamalizika; na mwaka huu ambao tunaomba bajeti muipitishe, tunatarajia kutoa ajira kwa askari 3,117. Lengo ni kuhakikisha kwamba tunapunguza mzigo wa Askari wetu ambao wanatekeleza majukumu makubwa wakiwa na idadi ndogo. Askari wengi wanastaafu lakini Askari kwa muda mrefu walikuwa hawajaweza kuajiriwa hivyo pungufu hilo sasa linaenda kupungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo niliona nataka nilizungumzie ni kwenye eneo la mafunzo. Suala la mafunzo ni suala la msingi sana kwa vyombo vyetu vya usalama na katika hili nataka nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa maelekezo yake mahususi aliyotoa ambayo Waheshimiwa Wabunge mmeyapongeza ya kuhakikisha kwamba Askari ambao wanakwenda mafunzo hawakatwi posho yao. Hili limefanyika katika mwaka wa fedha huu ambao unamalizika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kusisitiza tena, katika mwaka huu wa fedha maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kuhakikisha kwamba hakuna Askari hata mmoja anakatwa posho yake ya aina yoyote kwa ajili ya mafunzo. Ndiyo maana katika bajeti yetu ya mwaka huu tumetenga zaidi ya Shilingi bilioni 29 kwa shughuli hiyo. Kwa hiyo, hakuna sababu yeyote kwa askari yeyote kukatwa posho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hakuna sababu yeyote kwa askari yeyote kukatwa posho. Lakini nipongeze wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama kuhakikisha kwamba wanaimarisha mafunzo vyuo vyetu vya kuwafundishia askari, na niipongeze vilevile Serikali kupitia Mheshimiwa Rais wetu kwa kutenga bajeti nzuri ya kuimarisha miundombinu ya vyuo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningetoa mfano wa Chuo cha Zimamoto na Uokoaji mwaka huu wa fedha tunavyozungumza tuna takribani bilioni 1.1 lakini kazi nzuri inaendelea kukamilika katika Chuo cha Raphael Kubaga cha Uhamiaji kule Tanga vilevile, na upande wa Jeshi la Polisi halikadhalika. Kwa hiyo katika eneo la mafunzo kuna jitihada kubwa ambazo zinaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika eneo la uimarishaji wa miundombinu ya usafiri, nimezungumza katika bajeti hii kuna fedha ambayo tumetenga takriban milioni. Kwanza nizungumze, katika bajeti iliyopita mtakumbuka kwamba nilieleza bilioni 15 ilitengwa na kufedha ambayo tayari imeishatolewa kununua magari hayo, na mwaka huu wa fedha tunatarajia kununua magari mengine 24 zaidi kwa shilingi bilioni 7.6. Lakini magari ambayo yako njiani kufika ni magari 101 366 ni pikipiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia kuhusu umuhimu wa kuimarisha usafiri katika ngazi za chini za Kata. Lakini si katika suala la usafiri tu, mwaka huu tumekuja na mpango kabambe. Mheshimiwa Naibu Waziri alizungumza hapa, kwa mwaka jana mtakumbuka tulizindua mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba tuna kabiliana na changamoto ya usafiri, makazi ya askari kwa vyombo vyote vya ulinzi na usalama ambapo lengo lilikuwa ni kuja na nyumba na vituo vya polisi 51,760. Tumefanya mpango huo kwa mafanikio makubwa kwa mwaka huu mmoja. Hata hivyo tumeona kuna haja ya kuupitia tena mpango huo na kujikita zaidi katika ngazi ya chini. Baada ya kuona mafanikio makubwa ya Askari Kata katika kata zetu ambapo wamekuwa wakifanya kazi kubwa sana, wamekuwa wakifanyakazi ya kutoa elimu na kuelimisha, wamekuwa karibu na wananchi na kuweza kuyakabili matukio kwa haraka yanapotokezea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge kwahiyo nawapongezeni sana kwa jinsi ambavyo mmeona juu ya umuhimu wa kuwawezesha askari wetu kata hawa, ambapo kata hizi zipo katika majimbo yenu yote. Ndiyo maana tukapewa maelekezo na Mheshimiwa Rais ya kuhakikisha kwamba si tu tunapeleka magari katika wilaya lakini tupeleke pikipiki katika kata zote ambako kuna askari kata. Na gari na pikipiki hizi ambazo ziko njiani zitakapofika tutaanza kuzitawanya katika kata na Wilaya hizo. Si tu pikipiki na magari, hata mafuta yatakwenda sasa moja kwa moja kwenye kata na Wilaya, hayatabakia Mkoani. Na ukiangalia bajeti hii imeonesha kiasi cha fedha ambacho kimetengwa kwa ajili ya mafuta kimeongezeka kwa kiwango kikubwa sana (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama hiyo haitoshi, kwa eneo hili la kata tumeweza kufanya maboresho makubwa sana ya Mfuko wetu wa Tozo na Tozo. Kama mnvyotambua Mfuko wa Tuzo na Tuzo umekuwa ukifanya kazi kubwa sana ya kuchangia jitihada za kuimarisha vituo vya polisi na nyumba za askari ili kutoa msukumo zaidi na nyongeza ya kazi kubwa ya fedha ya bajeti ya Serikali inayotengwa kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu nichukue nafasi hii kumpongeza IGP kwa kuweza kutoa msaada mkubwa sana katika kufikisha azma hii ya kuleta maboresho makubwa katika matumizi ya mfuko wetu wa Tozo kwa kushirikiana na Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Polisi. Tunakwenda kufanya maboresho makubwa ambayo yatapelekea sasa kuhakikisha tunapata fedha za kujenga vituo vya polisi vya kata zote nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako Wabunge mbalimbali ambao walizungumza hapa, nimeandika majina yao, wale ambao walikuwa wamezungumzia kuhusu habari ya vituo vya polisi kata. Walisema wameishaanza hizo kazi za kujenga vituo vya polisi kata katika kata zao lakini vimeshia njiani kabla ya hata mpango huu. Niwapongeze, najua na wengine hamjapata nafasi ya kusema, lakini mmefanya kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge hawa nitakao wataja wamefanya. Mheshimiwa Chaya, Mheshimiwa Iddi, Mheshimiwa Vicent, Mheshimiwa Jah People haa hili jina nadhani halina shida Mheshimiwa, Mheshimiwa Nicholas, Mheshimiwa Munira, niliwasikia mkizungumzia habari ya vituo vya kata. Nataka niwahakikishie, kwamba tutakapoanza kutekeleza mpango huu najua yatahitajika mabadiliko ya sheria, lakini tutaharakisha. Tunadhani katika kipindi kisichozidi miezi sita tuanze utaratibu huu. Tutaanza na kata zenu na tutaanza na kata zile za Waheshimiwa Wabunge ambao watakuwa wameenda kwakushirikiana na wananchi wao kuanza jitihada za kutafuta maeneo na kuanza kazi za awali. Hilo nataka niwahakikishie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nadhani tutakapoweza kufanikiwa kuweka miundombinu imara katika kila kata katika nchi hii hali ya usalama itaendelea kuimarika katika maeneo yenu na hatimaye katika Taifa kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya Magereza ameyazungumza vizuri Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa hiyo mengine ambayo niliona niyachangie ni kwamba, kuna hoja ambazo zimezungumzwa kuhusiana na suala la uhamiaji haramu, lakini wengine wakalinasibisha jambo hili na msongamano wa mahabusu. Wamesema kwamba wahamiaji haramu hawa wako wengi, hususani hawa ambao wanatoka nchi ya Ethiopia, wamekuwa wakijaza magereza na hivyo kusababisha msongamano. Sitaki nikatae, changamoto ya Wahamiaji haramu hususani wa Ethiopia kwa kwakweli ipo, ingawa imepungua kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti naomba nieleze takwimu mpya ambazo tunazo sasa hivi tunavyozungumzwa. Wahamiaji haramu waliyopo sasa hivi katika magereza ni 1,600. Tumefanikiwa kuwaondosha wahamiaji haramu 3,100 katika siku za hivi karibu. Tumefanya hivyo kwa jitihada na ushirikiano na msaada kwanza wa Shirika, nichukue fursa hii kulishukuru sana Shirika Uhamiaji la Kimataifa (IOM) kwa kuweza kutusaidia kuwasafirisha wahamiaji haramu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nipongeze jitihada ambazo zimeendelea kufanyika kwa ushirikiano wa Idara yetu ya Uhamiaji pamoja na Ubalozi wa Ethiopia hapa nchini kwa kuhamasisha ndugu wa hao wahamiaji haramu katika nchi yao kuweza kutoa fedha za kuwaondoa. Jambo hili limetusaidia sana kama Serikali kupunguza gharama za kuwasafirisha watu hawa ambazo hazina sababu yeyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua mna uchungu sana, kwamba watu hawa wakikaa magerezani wanakula bure. Lakini watu hawa vilevile tukitoa hela za wananchi ambazo zingeenda kujenga shule, zingeenda kujenga hospitali, tukawasafirisha watu ambao waliyokuja hapa kwa hiyari na yenyewe vilevile ni kutumia rasilimali vibaya. Ndiyo maana tukaamua kutuma jitihada hizi; jitihada za kuhakikisha kwamba tunazungumza na Shirika la IOM watusaidie kuwaondosha na wamefanya hivyo na kuzungumza na ndugu zao ambao wamefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la muhimu zaidi ni nini ilhali unaweza ukawaondosha leo wakaja wengine kesho? Jambo la muhimu ni kuhakikisha kwamba tunatafuta ufumbuzi wa kudumu la tatizo la kudumu la Wahamiaji haramu ususani ambao wanatoka Ethiopia ambao ni wengi. Katika kufanya hivyo, katika Hotuba yangu nimesoma imeeleza kwamba, tumefanya marekebisho ya kanuni na kuiondoa nchi ya Ethiopia kutoka katika listi ya nchi ambazo zinatumia viza rejea. Sasa hivi raia wa Ethiopia anaweza akaja na passport yake akaingia kwenye mpaka, akatoka bila ya bughudha yeyote. Jambo hili limesaidia sana kutupatia ufumbuzi wa kudumu. Najua ni mapema mno kuweza kusema tunajivunia kwa kiasi gani. Lakini tunavyozungumza sasa hivi takwimu zinaonyesha kwamba tunapata wahamiaji haramu kutoka Ethiopia kwa mwezi hawazidi 40, wakati ilikuwa kwa mwezi wahamiaji haramu zaidi ya 300 wanaingia nchini. Kwa hiyo ni dhahiri kwamba utaratibu huu umeweza kusaidia na pengine utaweza kusaidia zaidi kuliondosha kabisa kama siyo kulimaliza tatizo la wahamiaji haramu katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la msongamano wa Mahabusu lina mambo mengi; na ndiyo maana nataka nichukue fursa hii tena, mimi leo sisemi mnyonge maana Mheshimiwa Rais hawezi kuwa mnyonge; nitasema tumpe haki yake Amiri Jeshi Mkuu kwa jinsi ambavyo anaguswa na changamoto za vyombo vyetu lakini na wananchi wa nchi hii ambao wanahitaji huduma kwa vyombo hivi. Kitendo chake kwa kuunda Tume ya Haki Jinai ambayo hivi karibuni itawasilisha ripoti tunategemea Tume hii itakuja kutupa mapendezo mengi ikiwemo hayo mliyoyazungumza, maboresho ya haki na stahiki za askari, masuala ya mafunzo ambayo nimeelezea na mengineno, lakini hata utaratibu wa jinsi ambavyo mifumo na miundo ya Taasisi zetu za Haki Jinai. Kwa mfano katika jambo moja ambalo lilikuwa lina changia ongezeko la Magerezani kuwa na msongamano, kama ambavyo mnajua, kuna idadi kubwa ambayo inakaribia idadi ya wafungwa ya mahabusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo unaweza ukakabiliana na tatizo la kuondosha wafungwa ambalo tunakwenda nalo vizuri. Mheshimiwa Rais amefanya jitihada kubwa ya kutoa msamaha kwa wafungwa nimetoa Takwimu, wakati ambapo nawasilisha taarifa yangu. Amefanya kupitia Katiba katika Ibara ya 45(1)(c) cha Katiba kimempa Mamlaka Mheshimiwa Rais ya kutoa msamaha wa wafungwa ambao katika kipindi kilichopia wafungwa 12,515 wameweza kutolewa, kwa mwaka 2017. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hizi taarifa zisiingie kwenye Hansard lakini nataka tu mtambue tu kwamba kuna Idadi kubwa ya wafungwa katika kipindi cha kuanzia miaka hiyo ambayo tangu utaratibu huu umeanza wa wafungwa kuachia. Pia kana kwamba hii haitoshi kupitia Sheria ya Bodi ya Parole Sura Na. 400 inazungumzia wafungwa 1,046 ambao wameachiwa lakini kwa huduma ya jamii inazungumzia wafungwa 5,339 ambao wametumikia vifungo vya nje pamoja na kufaidika na huduma hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo utaona, takwimu hizi zinaonyesha jinsi ambavyo sheria hizi; Sheria ya Bodi ya Parole, Sheria ya Huduma ya Jamii pamoja na Sheria ya Kifungo cha Nje, pamoja na Mamlaka ya Mheshimiwa Rais Kikatiba inavyosaidia kutupungumzia msongamano wa wafungwa magerezani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hii haigusi maabusu. Kwa hiyo lazima kuna haja ya kuangalia namna ya kufanya ili kuhakikisha kwamba tunawaondoa na kuwapunguza mahabusu katika Magereza; na ndiyo maana nimezungumza hapa suala la Tume ya Haki Jinai ambayo naamini kabisa itakuja na mapendekezo ambayo pengine yatatusababishia tuweze, sitaki nilisemee, lakini najua, kwa sababu hata sisi kuna mambo ambayo tumeyaona na tumeyatolea maoni na tutaendelea kuyatolea maoni ili yaweze kuingizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni namna ambavyo utaratibu wa jinsi mifumo na miundo yetu itakavyoharakisha masuala ya upelelezi, kuepusha mianya ya kutokuwa na upelezi usiokuwa na mapungufu. Wakati mwingine unaweza kusema sasa hivi tumejitahidi sana, Jeshi la Polisi limejitahidi. Kwa mfano ukienda Magereza leo hakuna hata mahabusu mmoja ambao upelelezi wake haujakamilika, lakini bado kuna msongamano. Kuna mahabusu ambao pengine bado wako ndani kwa sababu tu ya sheria zetu zilivyo, kuna mahabusu ambao wako ndani pengine wamekosa dhamana kwa kushindwa kutimiza vigezo vya dhamana, kuna mahabusu pengine wapo ndani leo kwa sababu wanamakosa ambayo kwa mujibu wa sheria hawapaswi wapate dhamana. Kuna mahabusu wapo ndani kwa utashi wao tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mambo haya yanahitaji ufumbuzi wa pamoja, na ndiyo maana nichukue fursa hii kupongeza sana ile Kamati ya Haki Jinai, ambayo iko chini ya DPP ambayo imekuwa ikipita kwenye Magereza mbalimbali na kupitia kesi za mahabusu moja baada ya nyingine na kusaidia wale ambao pengine walikuwa wanahitaji msaada wa kisheria, msaada wa mawazo, na wengine ambao kwa sababu ya uelewa mdogo wameshindwa kuzifahamu haki zao; na mahabusu wengi wamekuwa wakiachiliwa kwa utarabu huo. Kwa hiyo niliona nizungumzie hizo ni kama sehemu ya jitihada ambazo tunazichukua za kuhakikisha kwamba tunapunguza msongamano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaendelea kuimarisaha Magereza yetu. Wakati nchi hii inaundwa idadi ya watu walikuwa ni wachache sana, sijui kama bado walikuwa wanafika milioni 12. Sasa unazungumzia watu milioni sitini na kitu. Kwa hiyo lazima maeneo haya haya ambayo tumerithi kutoka kwa wakoloni tukubaliane ukweli kwamba hayawezi kutosha kulingana na idadi ya watu walio hapa. Na ndiyo maana katika bajeti yetu mwaka huu tumeongeza. Mwaka jana tulitenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Magereza sita na fedha yote hiyo imetoka na kazi inaanza, mwaka huu tumeongeza Magereza 12. Tunaamini kabisa tutakajenga Magereza mengi zaidi na kuongeza mabweni si tu itasaidia kupunguza msongamano lakini itasaidia dhamira tuliyokuwa nayo katika kuhakikisha kwamba kwenye hii hoja ya maboresho tuanayoendelea nayo katika Wizara ya kuangalia utaratibu wa urekebu ili tuhakikishe kwamba wafungwa wanaotoka magerezani hawarudii makosa. Na moja katika jambo ambalo linasaidia kuwa na urekebu uliyo bora ni mazingira mazuri ya wafungwa hawa wanapokaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano ukiwa na magereza ya kutosha yenye nafasi utaweza kutenganisha wafungwa kulingana na uzito wa makosa yao, usugu wa uhalifu waliyokuwanao umri na kadhali. Kwa hiyo hoja hii ya ujenzi wa Magereza ni hoja ya msingi na hoja endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine ambalo limezungumzwa vilevile, naomba niliunganishe hapa hapa; hoja ya kuimarisha vitendea kazi. Hakuna namna ambavyo tunaweza tukaimarisha usalama wa nchi katika karne hii bila kuwa na vyombo vya kisasa; ikiwemo Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza, Zimamoto na Jeshi la Uhamiaji. Na ndiyo maana niungane sana na Waheshimiwa Wabunge ambao mmezungumza kwa uchungu sana kuhusu eneo la Jeshi la Zimamoto na Uokoaji. Mmezungumza kwamba Jeshi hili limesahaulika, Jeshi hili linaonewa, wako ambao waliofikia wakasema kwamba kuna haja ya turudishe kwenye Halmashauri, wamesahau changamoto zilizotokea wakati huo ambazo zilikuwa zinasababisha ikaletwa kwenye Jeshi. Lakini najua mmesema hivyo kwa sababu ya uchungu mlio kuwanao, ambapo mko sahihi kabisa, wala mimi siwezi kuwa Waziri ambaye nasema uongo hapa mbele ya Bunge, nikasema kwamba eti Jeshi la Zimamoto letu liko vizuri, lina vifaa vya kutosha; nitakuwa ni Mbunge mwongo, Waziri mwongo na siwezi tena kuingia kwenye rekodi hiyo. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, nakubaliana na ninyi juu ya kilio chenu hicho. Lakini Waheshimiwa Wabunge nataka niwaambie kitu kimoja; kwamba mkipitia bajeti yangu niliyoisoma mtagundua kuna maeneo mawili ambayo nimeyaeleza na maeneo hayo nadhani yanakwenda sasa kutupatia suluhisho la kudumu kwenye matatizo ambayo ninyi yanawaumiza kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa jambo la kwanza, kwamba tunatarajia kupata magari ya Zimamoto 12 hivi karibuni kupitia mkopo wa masharti nafuu kutoka Serikali ya Austria. Nadhani hii nyimbo ya mkopo huu wa Austria ni ya miaka mingi sana, na ninyi Waheshimiwa Wabunge mtakuwa ni mashahidi. Hakuna siku nilivyokuwa Naibu Waziri katika miaka yangu mitano sikuwa nimeimba mwimbo huu; lakini leo santuri hii inafikia mwisho, hayo magari yapo njiani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa zaidi ni kwamba, kupitia Wizara ya Fedha na Mipango Serikali inakamilisha mkopo mwingine wa masharti nafuu. Nichukue fursa hii kumpongeza tena Mheshimiwa Rais, kwanza kwa kuimarisha demokrasia ya uchumi. Ndiyo maana leo tunazungummzia mikopo hii mizuri kabisa ambayo haitakuwa mzigo kwa Watanzania, lakini inakwenda kutoa na kuongeza thamani ya maisha yao na uhai wao, maana uhai uwezi kununua kwa hela na pia inakwenda kuokoa mali zao. Kama mlivyosema Waheshimiwa Wabunge mlio wengi; kwamba leo hii nchi imefunguka, wawekezaji wanaongezeka. Mmeona takwimu nilivyoisoma kwenye Uhamiaji, jinsi idadi ya watu wanaoingia, jinsi vibali vya class A vilivyozidi kiwango, inadhihirisha kwamba sasa kuna wimbi kubwa sana la uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa na uwekezaji mkubwa halafu tuwe na Jeshi la Zimamoto kama tulilo nalo sasa hivi. Lakini kupitia mkopo huu ambao nina imani kabisa upo katika hatua za mwisho tutakuwa na Jeshi la Zimamoto la kisasa. Kama tulipata shida sana kuzima moto uliokuwa unawaka Mlima Kilimanjaro sasa hivi tutakuja kuleta helkopta kwenye Zimamoto mkopo huu ukikamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, kwamba Serikali ya Awamu ya Sita imeliona hilo na Insha Allah kwa uwezo wake Mwenyezi Mungu jambo hili litakwenda vizuri na litakwenda kuondosha changamoto ambazo Wabunge wamezieleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo ni mengi, najua nimeletewa hapa note kwamba nimalizie, lakini nataka nizungumzie uraia pacha. Hili nililizungumza juzi, majibu yangu yanabakia vile vile kwamba waheshimiwa ni Watanzania wenzetu ambao wako nje, tunawathamini sana, michango yao ni muhimu, hapa ni nyumbani kwao japokuwa wameamua kwenda kuchukua passport nyingine kwa sababu zozote waliokuwa nazo, tunawahitaji sana waweze kuja kutoa michango kwa uchumi wa nchi hii. Ndio maana Serikali kwa kupitia Wizara ya Mambo ya Nje, ilifanya majadiliano nao na wakaona kwamba kwa sasa na kulingana na uhitaji uliopo, wanaweza wakatimiza azma yao hiyo kwa kuweza kupewa hadhi maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana katika hotuba yangu hii nimeeleza juu ya mpango wa marekebisho ya sheria nyingi ikiwemo Sheria ya Uhamiaji, Sura ya 54 ambayo inalenga kwenda kutibu tatizo na kero moja kubwa ya watu hawa, ili kuwa wanaingia hapa kama wageni, lakini sasa kama jambo hili litapita, basi wataingia hapa bila visa, wataingia hapa kama anavyoingia Mtanzania mwingine. Kwa hiyo hiyo ndio kauli yangu, nasisitiza katika hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona amenitoa katika mstari nilikuwa nataka nieleze kitu kimoja cha muhimu sana, kwamba hii dhana ya maboresho na kuwa na vyombo imara, nikisema hapa nizungumze mipango na mikakati ambayo aidha imeshafanyika au inaendelea kufanyika nahitaji muda mwingi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo nataka niyagusie ambayo Waheshimiwa Wabunge mmeyazungumza kabla sijamaliza. Wamezungumzia hoja ya kuwa na umuhimu wa kuwa na mifumo ya kisasa ya kubaini kushughulikia, pamoja na kuzuia uhalifu ikiwemo kuweka mifumo ya miji salama. Nimezungumza katika hotuba kwamba tunaenda sasa kuweka kamera kwenye miji yetu mitatu kwa kuanzia, lakini nimezungumza najua kuna Waheshimiwa Wabunge wana changamoto hata Mheshimiwa Makamu Mwenyekiti kwenye Kamati alikuwa analizungumza sana hili na tatizo pamoja na Mheshimiwa Aida kule Nkasi kwenye Maziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikwenda juzi kwa Mheshimiwa Chege, tatizo hili la vifaa, boti kwenye Maziwa yetu kwenye Bahari, kwenye bajeti hii kuna boti 10 tunaenda kununua. Kwa hiyo mambo ni mengi, lakini kwa sababu muda ni mchache naomba nimalizie labda jambo moja tu ambalo nisingeomba niliache kutokana na jinsi ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamelizungumza kwa hisia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la NIDA. Ni kweli tumekuwa na changamoto kubwa kwenye upatikanaji wa vitambulisho na changamoto hiyo ilitokana na sababu nyingi. Kwanza, ilikuwa, hatukuweza kununua kadi ghafi za kutosha kwa wakati, lakini sababu ya pili ilichangiwa na kutokea mambo ya UVIKO, tuliweka fedha kwa ajili ya kuomba hizi kadi na mlolongo wa foleni ya mahitaji ulikuwa mkubwa, ikawa tumechelewa kuzipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichukue fursa hii kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na wananchi wanaonisikiliza hapa, kwamba fedha zote za kadi na ziada zimeshalipwa, yaani sasa hivi hatuna deni la kadi hata moja. Kwanza tulitoa bilioni 28 ambazo kadi zake ziko njiani na nyingine zimeshaanza kuingia nimeambiwa mpaka mwezi huu kuna kadi zimeingia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunakwenda kukata mzizi wa fitina. Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati amezungumza vizuri, tunakushukuru Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kulieleza vizuri Mheshimiwa Vita Kawawa. Shilingi bilioni 42.5 na hii ndio fedha ambayo tulitenga kwenye bajeti ya mwaka jana kwa ajili ya ununuzi wa kadi. Maana yake ni kwamba tumetumia fedha ya ziada vile vile kupata kadi nyingi zaidi. Hivyo itakavyofika mwezi Desemba mwaka huu, tunategemea kadi zote zilizokuwa zimeshalipiwa zitakuwa zimefika na hivyo kuanzia wakati huo hatutarajii hata Mtanzania mmoja kuwa hana kitambulisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nisisitize kitu kwamba kwa hivi tunavyozungumza kwa wale Watanzania wenzetu ambao hawana ID hizi za NIDA. Najua wanazo zile namba za utambulisho waendelee kutumia namba hizo, namba hizo zinatambulika, namba hizo ni halali. Hakuna sababu yoyote ya kumkosesha haki yake Mtanzania yeyote popote pale alipo eti kwa sababu hana kipande kile cha NIDA. Kwa sababu namba hii inatumika na inaendelea kutumika kwa taasisi za Serikali, kuendelea kutoa taaluma na kuzitumia ili wananchi waendelee kupata huduma zao mpaka pale tutakapotarajia ambapo ni Desemba mwaka huu, kuwa tutaweza kufikisha kadi kwa wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana tukasema sasa tunataka tupeleke mwelekeo wetu kwenye ule utaratibu wa kuwa na kadi moja. Najua mchakato wake siyo mwepesi, lakini tutaanza nao. Tusingeweza kusema hivyo kama hata watu kadi zenyewe hawana. Inaleta matumaini sasa kadi watakuwa nazo, hivyo hata tukija na mpango kwa baadaye kwamba sasa tupunguze gharama za Serikali, za kuwa na rundo la makadi kwenye kipochi na kumsumbua mwananchi kupata huduma, tuwe na utaratibu huo wa kuwa na kadi moja kwa ajili ya matumizi ya huduma mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa fursa hii. Naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mimi sina shaka yoyote ju ya dhamira ya Waheshimiwa Wabunge katika hoja ambazo wamezizungumza na concern yao hususani kwenye kudhibiti fedha za umma. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba dhamira yao hiyo hiyo ndiyo dhamira ambayo Serikali yao inayo chini ya Uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nithibitishe kauli yangu hiyo kwa hoja zilizoguswa kuhusu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi katika Ripoti ya CAG na Waheshimiwa Wabunge pamoja na Kamati. Hoja kubwa ambazo zimeguswa ni hoja mbili.

Mheshimiwa Spika, nitaomba nichukue nafasi hii kuweza kutoa ufafanuzi huo kwa utaratibu wa kujiuliza swali mwenyewe na kujijibu mwenyewe. Wakati nitakapojijibu inawezekana ikawa inatosha kuweza kutoa ufafanuzi.

Mheshimiwa Spika, swala langu la kwanza nilikuwa nataka kujiuliza ni kwamba je sasa hivi, katika kipindi hiki cha Serikali hii wizi, ubadhilifu, ufisadi, unazidi, umekuwa mkubwa zaidi kuliko wakati mwingine wowote au kinyume chake?

Mheshimiwa Spika, hoja za CAG ambazo zimegusa Wizara yangu mbili. Moja ni hoja ambayo inahusu mfuko wa tozo na tozo na nyingine inahusu mfuko wa kufa na kuzikana. Majawabu haya ni vizuri yakajibiwa kwa facts and figures. Nikichukua hayo maeneo mawili ni maeneo ambayo yamegusa tuhuma nzito na kubwa sana na yametikisa chombo chetu muhimu sana kinacholenga kulinda usalama wa raia na mali zao hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kimetikisa heshima yake, kimetikisa heshima ya Taifa ya chombo hiki kikubwa. Sio jambo dogo hizi tuhuma na shutuma, lakini tuhuma na shutuma hizi hazijatokea kipindi hiki lakini zinarekebishwa kipindi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda tunaweza tukajiuliza kwamba kwanini tunafanikiwa maana mafanikio ni makubwa. Leo CAG inazungumza Ripoti kwa uwazi kama hivi, Bunge linazungumzwa kwa uwazi na uhuru wametuongoza vizuri kwa uwazi kabisa na uhuru wa hali ya juu.

Mheshimiwa Spika, hakuna Mbunge ambae umeacha kumpa nafsi. Haya ni mafanikio makubwa ya kujadili. Uwazi huu na mafanikio haya yana sababu zake na kila maji yanaanzia kwenye mkondo na samaki huanzia kwenye kichwa hatuwezi kuacha kumpongeza Amiri Jeshi Mkuu Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mkuu wa Nchi Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwezo wake mkubwa wa uongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni ishara ya uwezo mkubwa wa Kiongozi na ndiyo maana leo Taasisi zote muhimu zinafanya kazi zake nzuri kwenye Bunge hili, mihimili yote inafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya mafanikio ni kwa sababu Amiri Jeshi Mkuu ameweza kutafsiri vision yake ya wapi anataka Taifa liende kwa kuwapa imani, kuwa-inspire, kuwa-motivate vyombo na watu wanaoitwa mamlaka sisi tusimamie. Leo hii hata mimi katika Wizara niliyopewa dhamana sisubiri kusukumwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siwezi nikaona jambo lolote, doa lolote linajitokeza na tukaweza kulifumbia macho. Swali la pili je taasisi hizo mlizoziorodhesha chache TAKUKURU, Jeshi la Polisi na mengineyo na viongozi wanatimiza wajibu wao? Ama Serikali inalea wezi, serikali inalea wezi?

Mheshimiwa Spika, jambo moja ni muhimu sana Waheshimiwa Wabunge wakajua kwamba hoja hizi mbili na mimi nasema haya wazi kabisa na kama ninachokisema hiki nachozungumza hapa nitakuwa nashindwa kukitetea hakina ukweli, nasema mbele ya Bunge hili na wananchi wa jimbo langu wananisikia mimi niko tayari kuacha siasa.

Mheshimiwa Spika, nikiacha siasa maana yake Uwaziri haupo, Ubunge haupo ntarudi kwenda kushika spana. Lakini ninachokwambia ni kwamba haya ambayo tunayazungumza leo haya hayakutokana na uvumbuzi wa CAG, yametokana na maamuzi ya Serikali ambayo tulimwandikia sisi barua kufanya ukaguzi huu wa matatizo ambayo yametokezea kipindi kirefu nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ndiyo ilielekeza ukaguzi huu. Nihakikishe kwamba kila hatua anayochukua ni stahiki. Nachukua fursa hii kumpongeza CAG kwa kazi nzuri uliyofanya, nipongeze Bunge lako Tukufu na Waheshimiwa Wabunge kwa kujadili vizuri Ripoti hii ya CAG. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie, kama ambavyo tumeanza kuchukua hatua, nitazieleza hatua gani, na hatua ambazo hazijachukuliwa zitaendelea kuchukuliwa kwa kuzingatia maoni yenu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine la tatu ambalo nataka nilizungumze, hatua gani ambazo zimeshakuliwa dhidi ya wabadhirifu hao. Kwanza nataka nieleze kitu kimoja; CAG anafanana kidogo na polisi, sema yule anashiriki masuala ya jinai na yule anashiriki masuala ya kifedha. Polisi anapomkamata mhalifu anafanya uchunguzi, na akimaliza anapeleka kwa DPP, DPP, anaangalia uzito wa ushahidi uliokusanywa kama unajitosheleza kumpeleka mtuhumiwa mahakamani.

Mheshimiwa Spika, CAG anafanya uchunguzi wa kifedha kuangalia compliance ya matumizi ya fedha. Sasa leo hii tukisema mtu ambaye ametajwa, tena hajatajwa waziwazi katika Ripoti ya CAG aende jela hiyo sio misingi ya utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie, wale wote ambao wamethibitika bila shaka yoyote kuhusika wamechukuliwa hatua. Na nina orodha hapa, nina jedwali hili lina majina na hatua ambazo kila mmoja alizochukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda…

MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, watu ambao wamefikishwa mahakamani mpaka sasa hivi ni watu 18…

SPIKA: Mheshimiwa aliyesema taarifa.

MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Spika, huku taarifa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, watu ambao wamefukuzwa kazi ni…

SPIKA: Mheshimiwa Masauni, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ravia.

TAARIFA

MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Waziri; Ni kweli kachukua hatua lakini kwa askari wadogo tu, wale wakubwa bado wanaendelea kula maisha. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Masauni, unaipokea taarifa hiyo?

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, siipokei kwa sababu inaonekana Mheshimiwa Mbunge, alikuwa anasinzia wakati nazungumza, hakunisikiliza.

SPIKA: Hapana, ngoja, Mheshimiwa Waziri, hebu mwombe radhi Mheshimiwa Mbunge na ufute hayo maneno.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimefuta hayo maneno na nimemwomba radhi... (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, hizo ni tuhuma zote ya kwamba Mheshimiwa Mbunge alikuwa alisinzia. Anafuatilia mjadala ulioko hapa Bungeni. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa Spika.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, namwomba radhi swahiba wangu, Mheshimiwa Mbunge wa Makunduchi, tuelewane. Namwomba radhi na ninafuta, nina hakika hajakasirika kwa sababu ni rafiki yangu sana na anaelewa tunataniana mengi tu. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, baada ya kumwomba radhi Mheshimiwa Mbunge na kufuta kauli hiyo, naomba niendelee.

SPIKA: Mheshimiwa Masauni, ngoja, Mheshimiwa Ravia, naona bado umesiama.

MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Spika, naomba nimfahamishe Mheshimiwa Waziri kwamba, heshima ni kitu cha bure, lakini la pili ni kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PAC, ninachokiongea ninakijua kwa silimia mia. Kwa hiyo sijasinzia na ninachokiongea ninakielewa. Waliochukuliwa hatua ni wadogo na wakubwa bado wanaendelea kula maisha.

SPIKA: Haya, ahsante sana Mheshimiwa. Waheshimiwa Wabunge, nadhani kwa sababu Mheshimiwa Waziri wakati amesema ile sehemu yake ya mwanzo pengine kwa sababu ya zile kelele haikuwa imesikika, lakini mimi nilimwacha aendelee na mchango kwa sababu alishasema. Ameanza kwa kusema naomba radhi, huyu ni swahiba, kwa hiyo watu hawakusikia lile neno la naomba radhi nadhani ndiyo maana watu wameendelea na hizi kelele.

Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri ameomba radhi na amezungumza na hayo ya ziada, Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nimefikia kwenye takwimu za watu ambao wamechukuliwa hatua mbalimbali...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja, malizia mchango wako, kengele ya pili ilihsapigwa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, katika takwimu hizi za watu, kama ningesema nitaje majina ingeonekana ni wakubwa kiasi gani kwa maana tafsiri ya ukubwa ni pana sana lakini nina orodha ya watu waliofikishwa mahakamani, waliofukuzwa kazi na waliosimamishwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu ambao inasemekana walitoroka, lakini miongoni mwao hivi sasa wameshaanza kupatikana...

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: ...kuna mmoja amepatikana juzi, kwa hiyo kuna hatua nyingi ambazo zimeshachukuliwa kwa yale mambo ambayo yameshathibitika na hatua nyingine za kuweza kupata uthibitisho iliwaweze kuchukuliwa hatua zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka nizungume kwa haraka haraka…

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, ahsante sana.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Ni kudhibiti mifumo, ni kwamba, Je…

SPIKA: Mheshimiwa Masauni, muda wako umekwisha kengele ilikuwa imeshagonga nikakupa muda wa ziada. (Makofi)
Mapendekezo ya Nyongeza ya Bajeti ya Mwaka 2021/2022
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI K.n.y. WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nitumie fursa hii kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia na naomba niwatambue kama ifuatavyo; Mheshimiwa Subira Mgalu, Mheshimiwa Mtemvu, Mheshimiwa Halima Mdee na Mheshimiwa Kakunda. Naamini kabisa kungekuwa na muda wa kutosha Waheshimiwa Wabunge wengi walikuwa na haja ya kuchagia mpango huu mzuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba kama kuna siku ambayo nimewahi kusimama hapa kwenye Bunge lako tukufu, siku ambayo ni nyepesi kuweza kujibu hoja za Wabunge, hakuna siku ambayo imekuwa nyepesi kwangu kama leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu Waheshimiwa Wabunge takribani wote waliosimama na ukiangalia ambao hawajasimama jisnia ambavyo walikuwa wanagonga meza, basi inadhihirisha kwamba wale wachache waliosimama wamewakilisha mawazo ya wengi ambao hawajachangia, kwamba wana pongezi za dhati sana kwa kazi nzuri na ubunifu wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mambo mengi ambayo yamezungumzwa na kama Serikali tutayachukua ili tuweze kuyaendeleza ikiwa ni jitihada njema ambazo zimeanzishwa na Serikali hii ya Awamu ya Sita. Lakini kubwa zaidi, nimefarijika kuona Wabunge wengi na nyuso za furaha kwa sababu leo hii Wabunge hawa wanatembea vifua mbele majimboni kwao kutokana na miradi ambayo inaendelea ya sekta mbalimbali ambayo imetokana na fedha hizi za UVIKO. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na wako ambao waliwahi kusema kwamba haya yanayoendelea sasa hivi hayajawahi kutokea tangu nchi yetu imepata uhuru na tokea Mapinduzi ya Zanzibar na tangu Muungano wetu uliounganisha nchi hizi mbili. Kwa hiyo ni jambo ambalo linatupa faraja kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mawazo mengine ambayo yametolewa, ikiwemo umuhimu wa kuendeleza utaratibu huu wa uwazi na ushirikishwaji wa Bunge wa iwango cha juu, basi kama Serikali tumelipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo mengi yalikuwa ni pongezi; wako waliozungumza kwamba katika utaratibu wa kawaida nchi yetu sasa ni nchi ambayo ipo katika uchumi wa kati, hivyo basi kupata mkopo usiokuwa na riba ukifikia status hiyo ni jambo gumu. Lakini kwa jitihada za Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameweza kufanikisha mkopo huu tukaweza kuupata kwa riba zero kutoka riba ya asilimia 1.05 ya kiwango cha asilimia 66.6 ya mkopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo, nimeshangaa sana leo Mheshimiwa Mbunge mmoja hapa aliyezungumza, nadhani ni mawazo ambayo niliona kidogo yanahitaji kutolewa ufafanuzi pengine ilikuwa ni ambayo alizungumza Mheshimiwa Halima Mdee, kwamba leo anahoji kuhusiana na utaratibu wa mkopo huu.

Mheshimiwa Spika, hivi mkopo kama huu unawezaje kuhoji? Mkopo wenye neema kama hizi. Kama nitakuwa nimemuelewa sawasawa, lakini naamini kabisa na yeye anaunga mkono, lakini labda kama aliteleza kidogo ulimu basi nadhani nataka niliweke sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkopo huu ni mkopo wa bei nafuu na maisha yote kama nchi tunajaribu kukopa mikopo ambayo itakuwa nafuu ili kupunguza mzigo wa kulipa madeni kwa ajili ya mikopo kila mwezi. Pale ambapo yanapatikana mapato ya Serikali, fedha ambayo itatengwa kwa ajili ya matumizi itakapomalizika na fedha ambayo itatengwa kwa ajili ya kulipa madeni itakuwa imemalizika maana yake fedha ambayo itabakia itakuwa ni chache. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unapokuwa na mkopo ambao una muda mrefu wa kulipa kama huu maana yake unatoa nafuu ya kuweza kupata fedha za kuweza kutekeleza miradi mingi zaidi kwa sababu unapunguza matumizi. Lakini unapokuwa kwenye mkopo wenye riba zero kama huu maana yake una uwezo wa kulipa kidogo kwa sababu riba ni nafuu ama haipo kabisa. Kwa hiyo, niliona hili niliweke sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa ujumla Waheshimiwa Wabunge wamepongeza na zaidi ya pongezi sisi tunafarijika sana kwa jinsi ambavyo Bunge hili Tukufu limeweza kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais wetu za kuweza kuhakikisha kwamba mikopo kama hii tunaweza kuichangamkia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa zaidi ni jinsi ambavyo tumeweza kutumia mkopo huu kwa utaratibu ambao ni kinyume na nchi nyingi, kama Kamati ilivyosema kwamba nchi nyingi zaidi ya 40 ambazo zimeweza kupata mkopo huu hawakuweza kutumia kwa jinsi ambavyo sisi tumetumia kwa miradi ambayo ni ya kudumu na ya muda mrefu. Kwa hiyo niseme kwa ujumla kwamba yaliyochangiwa kwa ujumla ni hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache, sasa naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naafiki.