Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Boniphace Mwita Getere (111 total)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, asante. Kwa jina naitwa Boniphace Mwita ni Mbunge wa Jimbo la Bunda na ieleweke hivyo, mdogo wangu Ester Bulaya ni Mbunge wa Bunda Mjini.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo ya Jimbo la Bunda yanafanana na matatizo ya Nkasi, kuna Kata ya Unyari, ambayo ina vitongoji vyake na maeneo yake, ambavyo ni Nyamakumbo, Manangasi, Magunga, na Nyamatutu, na kijiji cha Kihumbu vitongoji vyake na Kihumbu na Mwimwalo vina tatizo lile lile la kutokuwa na mawasiliano, na kwa kuwa maeneo haya yana wakulima wengi na wafugaji wengi, na kwa kuwa wakulima hawa wako kwenye hali hatari ya tembo.
Je, Mheshimiwa Waziri haoni kuna umuhimu sasa wa kupeleka mawasiliano maeneo hayo ili wajiokoe na hali ya ulinzi wake na pia kwa mawasiliano ya kawaida?
Kwa kuwa wananchi hao wamechoka kuahidiwa na leo wamekuja hapa Bungeni kuonana na Waziri kuhusiana na maeneo yao hayo.
Je, Waziri yuko tayari kuonana nao leo? (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumhakikishia Mbunge kwamba nitakuwa tayari ofisini tuonane tu-discuss masuala yote aliyoyaongelea na tumpe takwimu sahihi.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante, tatizo la watoto au wanachuo wanaohitimu elimu ya diploma au stashahada ni kubwa mno. Haya mambo hayakuanza leo, toka mwaka 2007 wanafunzi wa Vyuo Vikuu kwa Taasisi ya TAHLISO wanadai hili suala halipo vizuri sana.
Kwanza vyuo vyenyewe vinapomaliza muda wake, muda wa kuhitimu masomo unakwepana na muda wa kusajili. Wanafunzi wanapopata ile wanaita supplimentary, kiswahili sijui; lakini na hawa wanachelewa kufanya mitihani yao kujiunga nao chuo. Sasa kama kweli majibu haya yako sahihi, kwanini bado wanapata matatizo haya?
Swali la pili, tatizo hili la kudahili wanafunzi wa diploma, wanapata shida sana kupata mikopo yao kwa maana vyuo vyao vinachelewa sana kupata vile vyeti na wao watu wa Bodi ya Mikopo hawapokei transcript ya mwanafunzi wa diploma. Sasa tunauliza, kwa kutumia hii Taasisi ya Elimu na kwa umaarufu wa Waziri, ndugu yangu Mheshimiwa Ndalichako na kwa kutumia ma-engineer…
NAIBU SPIKA: Naomba uulize swali Mheshimiwa.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Naam!
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la msingi ni kwamba naomba wanafunzi wanaomaliza stashahada wapewe nafasi ya kupata mikopo ya elimu ya juu, nalo ni tatizo. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni kweli kwa siku za nyuma kulikuwa na usumbufu kidogo ambao ulikuwa unajitokeza hususan kwa hawa wanafunzi ambao wanamaliza stashahada. Tatizo ambalo lilikuwa likijitokeza ni kwamba kwa upande wa wale ambao ni wanafunzi kwa mfano form six, wao matokeo yao yanakuwa moja kwa moja yanapitia Baraza la Mitihani ambalo ni moja, lakini kwa upande wa vyuo kumekuwa na utaratibu kati ya chuo na chuo kiasi kwamba baadhi ya vyuo vikuu vimekuwa haviamini kwa uharaka kwamba matokeo tunayoletewa ni sahihi. Kwa hiyo, walikuwa wanatafuta namna ya kufuatilia zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukaa pamoja na kuelezana uhalisia na kwa sababu matokeo hayo ya vyuo vilevile yanaenda kuhifadhiwa katika Hazina data za NACTE, kwa misingi hiyo hakuna huo usumbufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali hiyo, napenda nitoe agizo kwa vyuo vyote kwamba hakuna sababu ya kufanya usumbufu kwa wanafunzi hao ikizingatiwa kwamba matokeo yao yapo na yanaongea moja kwa moja na system ambayo inafanya shughuli ya udahili.
Kwa upande wa suala la udahili wa Stashahada kusababisha wanafunzi kushindwa kuingia katika nafasi za mikopo, kwasababu suala hili linalohusiana na mfumo, ni vyema tulichukue tuendelee kulifanyia kazi na hivyo tutashirikaiana na wewe mwenyewe Mheshimiwa Mbunge kupitia Kamati. Ahsante

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu wangu wa Elimu, ningependa kuchangia kidogo tu katika suala hili.
Kwanza napenda kutoa ufafanuzi kwamba mwanafunzi ambaye ana supplementary bado hajamaliza chuo. Mwanafunzi anakuwa amemaliza chuo pale ambapo anakuwa ame-clear mitihani yake. Kwa hiyo, mwanafunzi ambaye ana supplementary hawezi akadahiliwa kwenda katika chuo kwa sababu bado hajakamilisha masharti ya kumaliza elimu yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia kuhusiana na mikopo kwa wanafunzi wenye stashahada ya ualimu. Mwanafunzi anapata mkopo kulingana na vigezo vinavyowekwa na hivyo basi, kama mwanafunzi wa stashahada amekidhi matakwa ya kujiunga na elimu ya juu na anakidhi matakwa ya mikopo, hakuna usumbufu wowote unaotokea katika upatikanaji wa mkopo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujua tu ahadi ya ujenzi wa barabara ya kutoka Nyamwiswa – Bunda kwa kiwango cha lami ni ya muda mrefu toka mwaka 2000. Sasa napenda kujua ni lini Mkandarasi wa kujenga barabara hiyo ataanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumbukumbu yangu, hii barabara imeshaanza kujengwa. Tatizo kiwango tunachokijenga ni kidogo, labda ndiyo anachokilalamikia Mheshimiwa Mbunge. Nimhakikishie kama kumbukumbu zangu zitakosea atanisamehe, lakini kuanza tumeshaanza. Namwahidi tu kwamba, tutaongeza kasi ili hatimaye barabara hii ikamilike kujengwa katika muda mfupi.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, ni ukweli usiopingika kwamba zao la pamba bei yake ni ndogo mno ukilinganisha na uzalishaji wake. Ni lini Serikali itafanya mikakati ya dhati ya kupandisha bei ya pamba?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, hivi viwanda vidogo vidogo ambavyo kwa swali la msingi wamevitaja kwamba vitaanzishwa kwenye Wilaya ya Bunda hasa jimbo langu la Bunda ni lini vitaanza?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ikilinganishwa na nchi nyingine pamba yetu haipati bei nzuri. Hii inasababishwa pamoja na mambo mengine na ukweli kwamba wakulima wetu wengi wanauza pamba ikiwa ghafi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba wakulima katika vikundi vyao wanajengewa uwezo wa kumiliki viwanda vidogo vidogo ili waweze kuchambua pamba kwa sababu faida kubwa kwenye pamba ipo katika hatua nyingine za mnyororo kama kuchambua ambayo wakulima wetu hawashiriki. Hiyo kazi imefanywa na watu wachache. Kwa hiyo, tunataka tuwajengee uwezo waweze wenyewe kumiliki viwanda vidogo vidogo kama vya alizeti ili waweze kufaidika na mazao mengine yanayotokana na pamba kama mafuta pamoja na cotton seed.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile bei ya pamba inashuka kutokana na ukweli kwamba wakulima wetu wanakuwa na gharama kubwa za uzalishaji ikiwa ni pamoja na kununua pembejeo kwa bei ambayo ni ghali. Ndiyo maana Serikali imechukua maamuzi ya kuangalia namna ya kupunguza tozo na kodi mbalimbali zinazotozwa kwenye pembejeo ili kuondoa gharama kubwa za uzalishaji na hivyo baadaye wakulima wetu waweze kupata bei nzuri wakati wanapouza pamba yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, viwanda kama nilivyosema, mkakati wa kujenga viwanda vidogo, nafikiri mlishasikia bajeti ya Wizara ya Viwanda na Biashara, kwamba katika Awamu hii ya Tano tunataka kujenga uchumi wa viwanda na hasa viwanda vile vinavyotumia malighafi inayopatikana hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba pamba kama tungekuwa na viwanda vya kutengeneza nguo, kusingekuwa na haja hata ya kuhangaika ya kuuza pamba yetu nje. Kwa hiyo, ni kweli kabisa kwamba kuna mkakati mkubwa sasa wa kuhakikisha kwamba tunarudi kuwa na viwanda vya kutengeneza nguo ili pamba iweze kupata bei nzuri zaidi.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa kwa siku hizi za karibuni Watanzania wameshuhudia mauaji ya kutisha katika Mikoa ya Mwanza na Tanga. Je, Serikali ina mkakati gani wa dhati wa kuzuia mauaji haya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili lina majibu mapana sana kwa sababu linagusa vyombo kadhaa vilivyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani na hususan Jeshi la Polisi. Kwa sababu swali la msingi linahusu Idara ya Uhamiaji, naomba nilijibu kwa mtazamo wa Idara ya Uhamiaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Idara ya Uhamiaji suala la udhibiti wa uhalifu nchini inajikita zaidi katika kuhakikisha tunadhibiti uingiaji wa wahamiaji haramu nchini ambao mara nyingi wamekuwa wakihusishwa na kuongeza wimbi la uhalifu katika nchi yetu kwa kuingiza silaha pamoja na kujihusisha na vitendo mbalimbali vya uhalifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufanya hivyo, tumeandaa mkakati kabambe ambao utahakikisha kwamba unadhibiti vipenyo vyote vilivyopo mipakani. Mpaka sasa hivi tumefanya uhakiki katika baadhi ya mikoa na kubaini zaidi ya vipenyo 280 na bado tunaendelea katika baadhi ya mikoa ambayo hatujakamilisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatafuta fedha ili tuweze kufanya hiyo kazi ya kudhibiti mipaka yetu ili tuweze kuzuia hawa wahamiaji haramu wasiweze kuingia katika nchi yetu. Hata hivyo, tumekuwa tukifanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha kwamba tunawakamata wahamiaji haramu na kuwachukulia hatua zinazostahiki kwa kufanya misako katika maeneo mbalimbali nchini. Tumefanya kazi hiyo kwa mafanikio makubwa sana na wahamiaji haramu wengi tayari wameshakamatwa na wameshachukuliwa hatua za kisheria kwa kipindi kifupi tangu Serikali ya Awamu ya Tano ilivyoingia madarakani.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mimi naanza kutia mashaka kidogo kwenye miradi hii ya REA kwa sababu Waziri na Naibu Waziri wanasema mwezi wa sita ndiyo itakuwa mwisho wa REA Phase II lakini vijiji vyangu vya Jimbo la Bunda; Sanzati, Mikomahiro na Mihingo mpaka leo transformer iko moja kwenye Kijiji cha Sanzati na sioni kama kuna miradi inayoendelea pale, sioni kama kuna mafundi pale! Ni lini miradi hii itakwisha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, tulishakaa na Mheshimiwa Mbunge na tukajadiliana kuhusu vijiji vyake vya Sanzati na vingine. Vijiji alivyotaja Mheshimiwa Mbunge hivi sasa tunapoongea kazi inaendelea. Isipokuwa katika maeneo anayoyataja Mheshimiwa Mbunge nadhani vile vijiji sita kazi ambayo imebakia sasa ni kushusha nyaya chini kabla hawajawasha. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Bunda Vijijini na Bunda Mjini kwa ujumla wake vijiji vyote ambavyo viko kwenye ile Awamu ya II kama ambavyo inatekelezwa itakamilika ndani ya mwezi huu wa Juni.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo wananchi wasiwe na wasiwasi kwa vijiji ambavyo itaonekana kazi haitakamilika ndani ya mwezi Juni, tunaendelea kuifanyia kazi kuviwasha katika mradi wa REA Awamu ya III unaoanza Julai, 2016. Kwa hiyo, vijiji vya Bunda vyote vitapata umeme ifikapo mwaka 2017 kama mnavyotarajia.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, je, ni lini Serikali yetu sikivu itafanya tathmini ya hali halisi ya maeneo haya ambayo ukienda kwenye maeneo hayo kuona hali halisi; na kwa bahati nzuri katika eneo hili kwenye Bunge lililopita niliuliza swali na Waziri wa Kilimo enzi hizo, Mheshimiwa Mwigulu na Naibu mwenyewe nashukuru sana kwa kufika kwenye maeneo yangu; hali halisi ya eneo hilo halipo, watu wameshajenga. Sasa je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya hali halisi kujua maeneo haya ambayo wanamiliki hewa kumbe wananchi wote walishakali na kujenga shule za msingi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kutokana na Sheria Namba 17 na Namba 10 alizozitaja Mheshimiwa Naibu Waziri zimechelewa sana kwa wananchi wa Kijiji cha Mikomalilo, kwa sababu walishajenga na kulima mazao ya kudumu. Je, ushauri wake sasa haoni umechelewa sana ili kuwashauri watu walime mazao ambayo siyo ya kudumu?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu umuhimu na haja ya kufanya tathmini kuangalia hali halisi ya eneo la Holding Ground husika, Serikali inafahamu tosha kwamba ndiyo wananchi wamekuwa wakilitumia hilo eneo tokea miaka ya 1980; lakini kwa sasa hata pamoja na kwamba kuna maeneo ambayo yamevamiwa, hata yale ambayo yamebaki bado sisi tunaona kwamba ni muhimu kwa ajili ya matumizi ya Wizara na tusingependa kutumia kigezo cha kwamba kimevamiwa kuruhusu sasa; kwa sababu itamaanisha kwamba katika maeneo mengine wananchi vilevile wanaweza kuvamia.
Kwa hiyo, jitihada iliyopo sasa ni kuangalia namna gani tunaweza kunusuru maeneo yaliyobaki.
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, tukiruhusu maeneo yote ya Serikali yachukuliwe na wananchi baadaye Serikali ikihitaji maeneo tunaanza tena ugomvi na mgogoro na wananchi kwa sababu Serikali mara kwa mara itahitaji maeneo kwa ajili ya maendeleo ya kiujumla kwa ajili ya maendeleo ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, jibu hili la swali la kwanza la nyongeza, vilevile linajibu swali la pili kwamba tamko hili la kusema wananchi wasijenge, halijachelewa. Hata mwaka 1980 waliporuhusiwa, makubaliano ilikuwa ni kwamba wasipande mazao ya muda mrefu na wala wasijenge.
Kwa hiyo, wananchi wamekuwa wakifahamu na ndiyo maana hata Mheshimiwa Mbunge leo analiuliza hili swali wakati anafahamu kwamba huo ndiyo utaratibu uliokuwa ukitumika tokea mwaka 1980.
Kwa hiyo, sisi kama Wizara hatujachelewa, kilichotokea ni kwamba wananchi hawajafuata makubaliano ambayo tuliwekeana tokea eneo hilo lianze kutumika na wananchi mwaka 1980.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujua tu katika Wizara ya Maji kuna miradi sugu katika Jimbo langu la Bunda, kuna mradi wa maji Mgeta Nyang’alanga, Nyamswa Salama na kuna mradi wa maji Kiloreli na fedha zinazodaiwa Mgeta ni milioni 119 na Nyamswa ni milioni 229 na Kiloreli milioni 400. Naomba kujua tu hizi fedha zitaenda lini ili miradi hii ikamilike? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa katika Halmashauri ya Bunda Vijijini kiasi kumekuwa na matatizo na kuna miradi ambayo haijakamilika lakini pili, katika utekelezaji Halmashauri haijatuletea hati ili tuweze kulipa hiyo fedha. Kwa hiyo, nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mimi na yeye tutasaidiana kufuatilia kuangalia kuna tatizo gani kwenye hii Halmashauri. Kwa nini hii miradi imechelewa sana utekelezaji, kuna tatizo gani? Je, ni ni tatizo la kiutaalam au ni uzembe? Mimi pamoja na yeye tutalifuatilia hili kuweza kuhakikisha miradi hii inakamilika.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa Sheria ya Mazingira namba 20 ya mwaka 2004, Kifungu cha 182 na 183 (1) (2) na (3) na kifungu cha 36(1) na (2) tunatambua uwepo wa Maafisa Usafi na Mazingira katika Halmashauri zetu nyingi na kwa kuwa wahitumu hao wanamaliza elimu yao ya vyuo vikuu kwa vyuo vyetu hapa kwa wingi sana toka mwaka 1987, je, ni lini Serikali sasa itatangaza ajira ya wataalam hao ili kukidhi mahitaji ya mkakati aliyotaja Waziri? Swali la kwanza hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa maeneo mengi ya Nchi yetu mazingira yake yameharibika sana na kupelekea kuwepo ukame mkubwa na kusababisha njaa au uhaba wa chakula na hasa katika Jimbo langu la Bunda na Wilaya nzima ya Bunda. Je, Waziri yuko tayari kuitisha kongamano la kimazingira la kushirikisha Wabunge ili kujua hali halisi ya mazingira katika nchi yetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS-MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la Maafisa Mazingira; kama nilivyozungumza wakati nikijibu swali la msingi kwamba Maafisa Mazingira hawa tayari katika Halmashauri zetu wapo. Aidha, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge katika zile Halmashauri ambazo hawajaweza kuajiri watu hawa basi pale nafasi zitakapoanza kutolewa, Serikali itakapoanza kuajiri tena waajiriwe hawa wa Serikali zile Halmashauri zote zihakikishe kwamba zina Maafisa Mazingira katika Halmashauri husika kama maelekezo ambavyo yamekwishakutolewa. Lakini vilevile na Wizara zote ambazo hazina sekta hii ya mazingira wahakikishe kwamba wana hao maafisa katika sekta hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusiana na ukame ambao umepelekea uhaba wa chakula na Mheshimiwa Mbunge kupendekeza kwamba liwepo kongamano. Ninaloweza kusema kwamba wananchi wote na Wabunge wote ni lazima tukubali kwamba sasa tupo katika mabadiliko makubwa na tuko kwenye athari kubwa za mabadiliko ya tabianchi ambapo sasa inatupasa sisi sote kuhusiana na kilimo, kilimo chetu sasa hivi ambacho kimekuwa na mvua ya kusuasua kuhakikisha kwamba wananchi hawa wanaelezwa namna ya kutumia taarifa sahihi za wataalam wetu, tafiti zinazofanywa kulingana na mabadiliko ya tabianchi waweze kujua mbegu bora zinazohitajika kwa sasa hivi ili kupambana na huu uhimilivu wa tatizo la tabianchi, mbegu bora hizo zinazozungumzwa katika mazao hayo, lakini vilevile na mazao ambayo yanahimili ukame huo kulingana na mvua ambazo zinanyesha kwa kiwango cha chini sana sasa. Ipo mikoa iliyokuwa inapata mvua ambazo zinanyesha kwa kiasi kikubwa sana lakini leo hii mvua hizo zimekuwa za kusuasua, kwa hiyo, wananchi lazima wafundishwe hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu makongamano na taarifa mbalimbali za kuwahujisha wananchi; Hizo tutaendelea kuzitoa kwa wananchi ili waweze kuwa na tahadhari na hali hii ya sasa hivi ya mabadiliko ya tabianchi na suala la makongamano hilo litazungumzika kulingana na kwamba tumeshaamua kwamba shughuli yoyote ambayo tutaifanya tuhakikishe tunazidhibiti matumizi ya hovyo ya Serikali na hivyo tutahakikisha kwamba elimu hii tunaifikisha bila gharama kubwa sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuuliza maswali ya nyongeza mawili kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tatizo la upatikanaji wa
pembejeo kwa zao la pamba ni la muda mrefu sana karibu miaka 17 au 20. Ni lini sasa Serikali itakuwa na mikakati maalum ya kumaliza tatizo hili la pembejeo kwa wakulima wa pamba kwa sababu limekuwa sugu kwa muda mrefu?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni muda mrefu sana Serikali tumekuwa tukipandisha bei ya pamba kwa kutegemea soko la dunia. Ni lini sasa Serikali itatengeneza mkakati wa kupata bei ya wakulima wa pamba kwa kutegemea soko la ndani?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuboresha upatikanaji wa pembejeo za pamba. Hatua mojawapo ambayo imeshafanyika ni kuanzishwa kwa Mfuko Maalum wa Wakfu wa Pamba (CDTF), ambao kazi yake kubwa ni kugawa na kuhakikisha pembejeo zinapatikana kwa bei nafuu kwa wakulima wa pamba, kazi ambayo tayari imekuwa ikiendelea kwa miaka kadhaa sasa.
Mheshimiwa Spika, lakini vilevile Serikali inaendelea na mpango wa kuvifufua na kuboresha utendaji wa vyama vya ushirika ili viweze kusimamia upatikanaji wa pembejeo katika maeneo hayo. Jitihada hizi zinahusisha kwa mfano kufufua Chama cha Ushirika cha Nyanza ili kiweze kufanya kazi kuwasaidia wakulima wa pamba lakini vilevile vyama vingine kama SHIRECU, navyo vilevile kazi ya kuvifufua
inaendelea.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na namna gani Serikali inaendelea kuboresha soko la ndani, napenda kumtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba, mkakati tulionao kwa sasa
ni ule wa mwaka 2016-2020 wa kujaribu kuhakikisha tunaboresha mnyororo mzima wa thamani kutoka kwenye pamba hadi kufikia kwenye nguo. Katika mkakati huo, Serikali
inahakikisha kwamba tunajenga viwanda na kuhamasisha ujenzi wa viwanda ndani ili nguvu kubwa isielekezwe tena katika kutafuta soko la nje bali kutumia soko la ndani ambalo tunaamini tunalo. Kwa sababu kwa idadi ya Watanzania
iliyopo kama tutaweza kutengeneza nguo ambazo zitatumika ndani, tunaamini kwamba bei ya pamba itaendelea kuimarika.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Katika Jimbo langu la Bunda kuna vijiji vya Nyabuzume na Nyaburundu. Kuna wachimbaji wadogo wenye PL wa muda mrefu sana. Tatizo wale wachimbaji wanachimba, madini yanapatikana, lakini pale wanaambiwa kwamba wana leseni za utafiti. Serikali ya kijiji iliwaomba kutoa huduma za maendeleo katika maeneo hayo ya Nyabuzuma na Nyaburundu, hawataki kutoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua ni sheria ipi inawataka hawa wachimbaji ambao wanapata madini,
hawataki kusaidia vijiji hivyo vinavyohusika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa hakuna sheria inayowakataza
wachimbaji wadogo au wachimbaji wakubwa wasilipe levy au mapato yoyote yanayotokana na uchimbaji wao. Sheria ya Madini pamoja na Sheria ya Fedha inawataka walipe.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Getere kama kuna shida, wasiliana na sisi tukusaidie ili Halmashauri yako iweze kupata
fedha hizo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mimi nataka kuuliza kwa mtu ambaye ni Mtanzania aliyezaliwa katika nchi yetu, anayehoji juu ya Mwenge…
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Badala ya kuhoji juu ya mambo mabaya yanayotokea kwenye Mwenge, anayehoji juu ya Mwenge unafanya nini huyu unaweza kumkabidhi hii nchi akaendelea kukaa nayo? Nataka tu kupata ufafanuzi huo.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri ambalo linaonyesha jinsi alivyokomaa katika kujua historia ya nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu niwaambie Watanzania, falsafa ya Uhuru wa nchi yetu ya Tanzania haiwezi kutenganishwa na Mwenge wa Uhuru. Naomba niwakumbushe, wakati wa Uhuru tarehe 9 Desemba 1961, Marehemu Baba wa Taifa alisema, sisi tutawasha Mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro umulike ndani na nje ya mipaka yetu ulete amani, tumaini, upendo, uondoe chuki na dhuluma, sasa jambo hili si dogo. Kwa Mtanzania anayemuenzi Marehemu Baba wa Taifa itashangaza sana kama hatataka kuenzi falsafa ya Mwenge wa Uhuru. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda tu kuwaomba Watanzania kwa kweli hatuna haja ya kuchukuliana hatua ya namna moja au nyingine lakini wote tutambue Mwenge wa Uhuru ni tunu kubwa ya Uhuru wa nchi yetu na unapaswa kuenziwa na Watanzania wote.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Napenda kujua, kuna barabara ya Nyamswa –Bunda ambayo mwezi wa 12 mwaka jana alifika Mheshimiwa Profesa Mbarawa, Waziri na kuitembelea barabara hii na kuahidi kwamba ikifika Februari mwaka huu mkandarasi atakuwa site. Kwa bajeti inayoendelea sasa hivi, hiyo barabara ilitengewa bilioni nane. Sasa napenda kujua; ni lini mkandarasi atakuwa site kwa ahadi ya Waziri, kwa maana ya kwamba hii barabara ni ya muda mrefu kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi toka mwaka 2000?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara anazoziongelea ni kweli zipo katika mpango na fedha zimetengwa na tenda zimetangazwa. Nimwombe tu Mheshimiwa Getere kama ambavyo nimekuwa nikimwomba ofisini, maana amefuatilia sana ofisini, naomba tu yale masuala ya kutaka kupigana ayapunguze, lakini nimhakikishie kwamba kile ambacho nilimuahidi ndani ya ofisi tukiwa pamoja na Katibu Mkuu, tutayatekeleza.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ambayo nimepewa na Mheshimiwa Naibu Waziri kusema kweli sijui Bunda kuna nini hata nashindwa kuelewa. Kwa sababu unapotaja Kijiji cha Karukekere, Mumagunga, Kung’ombe, Ligamba na kama unavyotaja majibu kwenye paper ambayo nimepewa kwa maana ya kujibiwa kama Mbunge, yakaonyesha sehemu kubwa ya miradi inayotajwa sio ya Jimbo lako, hivi Mbunge unajisikiaje!
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nafikiri kwamba ni vizuri wakati fulani haya majibu, na nazani hili ni tatizo la Bunda tuna miradi mikubwa iko Bunda na Mabilioni ya hela, viongozi hawafiki pale kuona hela zinaliwa pale hawafiki, sasa naomba kuuliza niache kwa sababu leo ni siku nzuri tunaenda nyumbani tusilete shida huko mbele niseme sasa nimuulize Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuache haya ambayo ameyasema kwa sababu mimi sioni kama yako kwenye maeneo yangu, kuna kilometa nne za mradi wa maji mkubwa kutoka Ziwa Victoria huko Halmashauri jirani ya Butiama, sasa kama ni kilometa nne kuja kwenye maeneo ambayo yana uhaba wa maji ni lini Serikali itachukua mpango wa kuleta yale maji kutoka bomba la Ziwa Victoria kuja Nyamuswa, Bigegu, Tiring’ati na Malambeka?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa kuwa kuna mradi mkubwa ulikuja wafadhili kutoka SNV wa shilingi milioni 987 kuja Kijiji cha Nyamuswa na mradi ule unaonekana umefanyiwa ubadhirifu mkubwa sana ni lini Serikali itaenda kushughulikia wabadhirifu wa hela hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, miradi tunaitekeleza kihalmashauri, hatutekelezi kijimbo, sasa hii ndiyo maana inawezekana katika programu ya huo mradi ilichukua vijiji vingi vya Jimbo lingine na vijiji vichache vikawa vya Jimbo la Mheshimiwa Getere, lakini nikuhakikishie Mheshimiwa Getere kwamba utekelezaji unaendelea na mwaka huu tumeweka bajeti, kwa hiyo, tutaendelea ili kuhakikisha kwamba na vijiji vingi vilivyo sehemu ya kwako vinapata huduma ya maji safi na salama.
Mheshimiwa Naibu Spika, umezungumzia kwamba kuna vijiji kama Nyamuswa ambavyo viko kilometa nne tu kutoka ziwani, ninaomba tushirikiane na Wilaya yako tuangalie kwamba ni kitu gani kitafanyika japo katika swali lako la pili umezungumzia fedha zilizotolewa kutoka kwenye hii programu ya Lake Victoria Water and Sanitation Project na mradi huo mkubwa unaendelea kuzunguka Ziwa letu la Victoria. Kwa hiyo, tutaangalia ni namna gani sasa tutaweza tukaweka mradi mwingine kuupeleka maeneo haya ambayo umeyapendekeza. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge asiwe na wasiwasi tuko pamoja na tutahakikisha wananchi wako wanapata huduma ya maji safi na salama.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini hili tatizo la hizi kata limekuwa la muda mrefu na hasa ukizingatia kwamba kata zenyewe ziko pembezoni mwa Mji wa Musoma. Nataka kuuliza ni lini haya maji yatawafikia hizo kata kwa sababu wamekuwa na usumbufu wa muda mrefu?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, pamoja na matatizo ya mji wa Musoma pia kuna matatizo makubwa ya Mji wa Bunda na hasa Jimbo la Bunda ninakotoka mimi. Kuna kata saba zina matatizo makubwa ya uhaba wa maji ambazo ni Unyali, Kitale, Mgeta, Mihingo, Nyamaghunta na Salama; nilitaka kumuomba tu Waziri ni lini atafika? Nimuombe tu afike kwenye hizo kata saba za Jimbo langu ili aweze kujionea hali halisi ya uhaba wa maji katika jimbo hilo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; ni kweli kwamba, ni muda mrefu, lakini nimuahidi kwamba, mara mradi huu ambao umeanza kutekelezwa utakapokamilika wakazi hawa watafaidika na maji hayo. Swali la pili kuhusu Bunda; naomba nimuahidi Mheshimiwa Mwita Getere kwamba mara baada ya Mkutano huu wa Bunge nitatembelea Mkoa wa Mara na nitafika Bunda. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri ya kuridhisha, lakini naomba tunapouliza maswali haya tuwe tuna kumbukumbu ya majibu. Swali hili nimeshaliuliza zaidi ya mara ya tatu, katika bajeti ya mwaka 2017/2018 nimeuliza swali hili hapa Bungeni, Naibu Waziri wa Maji na sasa Waziri alijibu kwamba kwa mwaka wa bajeti 2016/2017 malambo haya yangefanyiwa ukarabati na bajeti ya Halmashauri ikaletwa hapa Bungeni sasa tena kipindi hiki wanasema bajeti itakuwa 2018/2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimshukuru Naibu Waziri wa Maji ambaye sasa ni Waziri alikuja kwenye Jimbo langu akaangalia miradi akamuuliza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya kwa hali iliyoko hapa Bunda unajua bajeti kiasi gani ya maji unayo. Mkurugenzi akasema haelewi, akatuambia ana bilioni 1.7 ya Halmashauri ya Bunda kwa ajili ya maji. Ni kwa nini hizi hela zisitumike kutengeneza haya malambo wakati yanahitaji shilingi milioni 350? Naomba Waziri atoe tamko la kutengeneza malambo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, tuna mradi mkubwa sana Mkoa wa Mara unatoka Mgango unakwenda Butiama lakini Vijiji vya Kata za Nyamswa, Kitare, Nyamamta na Salama viko jirani kilomita tatu kutoka kwenye mradi huu. Naomba Serikali ione namna gani inaweza kufanya vijiji hivyo viingie kwenye mradi mkubwa kutoka Ziwa Victoria. Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Getere kwa jinsi ambavyo anahudumia jimbo lake na alishawahi kunichukua tukaenda mpaka jimboni kuangalia matatizo ya miradi hii ya maji. Alichokisema ni kweli bajeti ya mwaka 2016/2017 Halmashauri yake hawakutumia hata senti tano, fedha yote ikarudi wakati wana matatizo ya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namwomba Mheshimiwa Jafo, Waziri wa TAMISEMI aniruhusu niagize Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bunda na Mwenyekiti, siku ya Jumatano wiki ijayo waje tukutane pamoja na Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kutatua matatizo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, tumetangaza tender kwa ajili ya kuweka bomba kubwa jipya la mradi wa Mgango-Kyabakari. Kwa hiyo, wakati wanaweka bomba hilo Mheshimiwa Mbunge nitaomba tuwasiliane ili tuweze kuainisha na hivyo vijiji vitatu alivyovisema navyo vipate maji kutoka Mgango. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, wakati fulani ni vizuri haya majibu nayo tukawa tunayaona vizuri kwa sababu, Mheshimiwa Mbunge anauliza Daraja la Mto Mori, Rorya. Majibu ya matumaini yanakuja Daraja la Mto Mori, Tarime inakuwa inapoteza ile ladha ya swali na hasa mtu anapokuwa ameuliza swali kwa muda mrefu katika Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka kujua Halmashauri hazina uwezo wa kujenga hili daraja ndio maana zimeomba Serikali Kuu isaidie kwa maana ya TAMISEMI. Ni lini sasa Serikali Kuu itatoa fedha za kusaidia daraja hilo kwa sababu Halmashauri ya Wilaya ya Rorya uchumi wake ni mdogo haiwezi kujenga hilo daraja?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Jimbo la Bunda ambalo natoka mimi kuna daraja la Mto Chamtikiti ambalo limeharibika muda mrefu na hivi karibuni tumesikia kwamba kuna fedha ilitoka kwa ajili ya kutengeneza daraja, lakini mpaka leo mvua inanyesha wanafunzi hawaendi shuleni kwa sababu ya hilo daraja. Ni lini Waziri atakuja Bunda kuliona hilo daraja kwa ajili ya kusaidia hali hiyo?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba niseme ni kweli nafahamu na mimi Mheshimiwa Getere unafahamu nilikuwa kule Rorya na pale changamoto ni kubwa. Na ni kwamba Halmashauri tunafahamu wazi kwamba kwa sasa haitaweza isipokuwa ni kwa kupitia mamlaka yetu tuliyoiunda ya TARURA.
Kwa hiyo, naomba niwahakikishie kwamba, suala zima la daraja hili na kwa sababu eneo hili ni eneo la kipaumbele, nitawaagiza wataalam wangu wafike katika daraja hilo, lakini na eneo lingine ambalo Mheshimiwa Getere ulilizungumza, lengo kubwa ni kwamba waende kufanya tathmini tujue thamani ya kazi halafu tutaangalia tutalitengeneza kwa kifungu gani. Aidha, kupitia DFAD kwamba eneo hilo saa nyingine ni eneo la vikwazo au kupitia Mfuko wa Barabara kwa kadiri itakavyoonekana inafaa, lakini nikuhakikishie kwamba, nitawatuma wataalam wangu wataenda kufanya study ya kutosha, lengo kubwa kuwasaidia wananchi katika maeneo hayo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Bunda na Vijiji vya Honyari, Kihumbu, Maliwanda, Sarakwa, Kyandege mpaka wao kati ya pori la Akiba la Gruneti na Mheshimiwa Naibu Waziri amesema hapa kutoka mpaka wa Mto Lubana kwenda kwa wananchi ni mita 500 ningependa kujua kutoka mpaka mto Lubana kwenda porini ni mita ngapi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa katika hili eneo la Gruneti kuna mipaka ambayo ipo lakini itakuwa ni vigumu sana kumpa taarifa kamili umbali uliopo kati ya huo mto na hilo eneo analolisema. Kwa hiyo naomba nitumie nafasi hii kuwambia kuwa nitakaa nae, tutaenda kutembelea hilo eneo ili tuone kwamba kuna umbali wa mita ngapi ambazo zinahusisha. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba tu kutoa ufafanuzi tena kwamba Wilaya ya Bunda ina Majimbo matatu. Kuna Mwibara ya Mheshimiwa Kangi Lugola; kuna Bunda Mjini kwa Mheshimiwa Ester Bulaya na kuna Jimbo la Bunda kwa Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri lakini naomba Mawaziri au Manaibu Waziri wanapokuwa wanapata hayo majibu kutoka kwenye Halmashauri wawe wanayatazama vizuri kwa sababu majibu ninayoyaona hapa yanahusu mpango wa Halmashauri siyo swali la Boniphace Mwita kwenye Jimbo la Bunda.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mimi nimeuliza mambo ya malambo unaniambia kuna gharama za kujenga mnada, sasa hainiletei faida kwenye swali langu hili. Naomba kujua tu, ni lini hizi shilingi milioni 90, shilingi milioni 200 na shilingi milioni 110 ambazo Naibu Waziri amezitaja kwamba zitatumika kukarabati na kujenga malambo hayo zitapelekwa Bunda na zitatoka chanzo gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, naomba kujua, malambo hayo sita ya kukarabati ambayo Naibu Waziri ameyataja hapa na matano ya kujengwa, yatajengwa vijiji gani? Maana naona kama hii ni jumla ya Wilaya ya Bunda yote.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, suala kwamba lini pesa hizo zitapelekwa ni kama nilivyosema katika jibu langu la msingi. Mheshimiwa Getere pia lazima akubali kwamba kama alivyosema awali kwamba Bunda ina Majimbo matatu, Bunda la Mjini, halikadhalika na Jimbo la Mwibara la kaka yangu pale Mheshimiwa Kangi Lugola, mipango yote ya fedha maana yake ninyi mnapokaa katika Halmashauri yenu ndiyo mnafanya maamuzi sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani Jimbo likatengeneza bajeti yake kama Jimbo isipokuwa kama Halmashauri ambayo ina Majimbo matatu ndiyo inapanga hivyo vipaumbele. Ndiyo maana katika jibu langu la msingi nimeainisha jinsi gani mlipanga mipango ya miaka mitatu katika ukarabati na ujenzi wa yale malambo mengine matano. Kwa hiyo, lini fedha hizo zitakwenda, ndiyo maana nimesema katika mwaka huu wa fedha mlianza kutenga bajeti ambayo kuanzia Julai ndiyo mwaka wa fedha huwa unaanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la pili kuweza kusema vijiji specific, Mheshimiwa Mbunge naomba niweze kusema wazi kwamba kwa hapa itakuwa vigumu kwa sababu Halmashauri imepanga mpango wake huu na kuainisha vijiji, nadhani tuwasiliane baadaye tuone jinsi gani tutafanya. Vilevile tuangalie na ninyi kule katika Halmashauri mpango mlioupanga mlisema mtatekeleza mradi huu katika vijiji gani.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie kwamba kilio cha Wanajimbo lake la Bunda kimesikika. Jukumu letu kubwa ni kuhakikisha sasa Wanabunda katika Jimbo lake wanapata mahitaji yale ambayo wanayakusudia. Mwisho wa siku kama wananchi wa kawaida au kama wafugaji wa kawaida basi waweze kupata maji kwa ajili ya malisho yao na matumizi mengine ya nyumbani.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa matukio ya Bunda yanazidi kuwa mengi kidogo, ni lini sasa Waziri au Naibu Waziri atatembelea Bunda ili kuona hali halisi ya mambo hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimuahidi kwamba tutashauriana na Mheshimiwa Waziri ili kati yangu ama yeye tuweze kwenda Bunda haraka iwezekanavyo. Tutakaa pamoja tushaurine ratiba hiyo ya kutembelea Bunda muda siyo mrefu sana. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya ndugu yangu Kangi Lugola nuru ya wanyonge, Jimbo la Mwibara, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa chanzo kikubwa cha maji ya binadamu, mifugo na wanyamapori katika eneo hili la vijiji tisa ni Mto Rubana, na kwa kuwa hakuna chanzo kingine mbadala kwa wananchi wa maeneo hayo, na kwa kuwa ardhi haiongezeki na watu wanaongezeka na mifugo inaongezeka. Je, ni lini sasa Serikali kwa kupitia Wizara yake ya Mazingira itapeleka mradi mkubwa wa maji katika vijiji hivi viwili ili kuviokoa na tatizo la maji?
Swali la pili, kwa kuwa Mto Rubana, ndiyo mpaka kati ya vijiji tisa vinavyopakana na pori hilo la akiba, la Grumeti. Je, ni lini agizo lako ulilolitoa miezi miwili iliyopita, ulipotembelea maeneo hayo kwamba mita 500 za eneo la wazi kutoka eneo la mpaka kwenda vijijini na mita 500 kutoka eneo la mpaka kwenda porini wataweka beacon?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Mheshimiwa Getere wapiga kura wako wanakuita Tingatinga la maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwamba baada ya uteuzi wangu nilitembelea Jimbo la Mheshimiwa Mbunge na kuweza kufanya mikutano miwili Maliwanda pamoja na Hunyari, ninamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali yetu tayari kwa kuzingatia kwamba wananchi walikuwa wanatumia maji ya Mto Rubana kunyweshea mifugo, uvuvi pamoja na matumizi ya nyumbani, tayari katika Kijiji cha Kyandege, Kijiji cha Mugeta na Kijiji cha Mariwanda Serikali tulishawajengea malambo ya kunyweshea mifugo na mabirika ya kunyweshea mifugo yanafanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna taasisi inaitwa Rubana Corridor Invironmental Development Strategy wako mbioni na wamekamilisha mchoro wa kujenga bwawa moja kubwa katika Kijiji cha Kihumbu. Pia Halmashauri ya Wilaya Bunda, katika mwaka wa fedha wa 2017/2018 wametenga jumla ya milioni 30 kukarabati lambo la Kihumbu na pia Foundation for Civil Society kushirikiana na asasi niliyoitaja mwanzo, tayari wanataka kujenga visima viwili vya maji katika Kijiji cha Kihumbu, ikiwa ni pamoja na kuongeza lambo moja kubwa kwa ajili ya kunyweshea mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuhakikisha uvuvi uliofanyika Rubana usiendelee na kuchafua mazingira, tayari Foundation for Civil Society wameendesha mafunzo ya vijiji vinne kwa ufugaji wa nyuki na sasa watasambaza mizinga 100 kwa ajili ya kuwafanya wananchi wasiende kuchafua mto.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu changamoto ya mita 500. Ni kweli kabisa Sheria namba 5 ya mwaka 2009 kifungu cha 74 kinazungumzia kuweka buffer zone ya mita 500 kwenda kwa wananchi. Nimhakikishie Mbunge tayari Ofisi ya Makamu wa Rais, imeshawasiliana na Mkurugenzi Mkuu wa TAWA pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii, kwamba wanashughulikia masuala ya beacon. Pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba beacon zinazohusu wanyama na wanadamu ni beacon ambazo siyo endelevu, leo utaweka beacon ya mita 500 kwa wananchi, na hawa wanyama wao hawajui kama kuna beacon ya mita 500, baadae watasogea tena kwenye mita 500, baadae wananchi watasema wanyama wamesogea tuweke tena beacon za mita 500, mwishowe vijiji vyote vitaisha kwa kuwa beacon ya hifadhi. Hiyo ndiyo changamoto iliyopo. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Bunda kuna miradi ya maji ya Nyamswa, Salama Kati, Mgeta, Nyang’alanga, Kiloleli, Nyabuzume, Kambugu na mradi wa umwagiliaji wa Maliwanda. Miradi yote hii ni ya muda mrefu sana. Nataka kujua tu Waziri kwamba hii miradi ambayo tayari mingi wameshaitolewa fedha na haijakamilika kwa muda mrefu, ni lini sasa hii miradi itakamilika?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni mara kama ya nne kuuliza maswali haya kwenye Bunge hili.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nikiri, sio kwamba amekuja mara nyingi tu lakini ameandika barua zaidi ya mara tatu kulalamikia utekelezaji wa miradi katika Halmashauri yake ya Bunda, na kwamba fedha nyingi zimepelekwa, sio na Wizara ya Maji tu, zimepelekwa fedha na Wizara ya Maji, zimepelekwa fedha na JICA shilingi milioni 207 nakumbuka, lakini kuna own source pia ya Halmashauri imetoka miradi ile haijakamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naona nitume watalaam wangu wa Wizara ya Maji waje kwako kuangalia hili baadae mimi pamoja na wewe tutakwenda kuangalia kuna tatizo gani, kama alivyosema Mwenyekiti pengine kuna shida ya makandarasi au kuna shida ya utekelezaji kwenye Halmashauri kama tulivyobaini katika maeneo mengine.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kuna mpango wa kujenga vituo vya afya 100 ambao tumeusikia kwa muda mrefu sana na mojawapo ni kituo cha kwangu cha Mgeta. Sasa ningependa kujua ni kigugumizi gani kipo mpaka sasa vituo vile havijaanza kujengwa wakati hela imetoka muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tuna mpango wa ujenzi na ukarabati wa vituo vya afya na miongozi mwa vituo hivyo ni Kituo cha Afya cha Mgeta. Naomba niwaambie kwamba mchakato sasa uko katika suala zima la evaluation, tulikuwa katika tendering process kwa sababu tuna vituo vingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge katika kipindi hiki cha mwezi wa Julai wataona ujenzi unaendelea katika maeneo mbalimbali ya vituo vile 100; then tutakuwa na program nyingine ya ujenzi wa vituo vipatavyo 42. Kwa hiyo, kuanzia mwezi wa Julai wananchi wa Mgeta watarajie kwamba, ujenzi katika eneo lao utaanza mara moja.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Waziri, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Katika nchi yetu raia wengi hawana vyeti vya kuzaliwa. Katika Mkoa wa Mara lipo kabila la jamii ya Waluo kwa maana ya Wajaluo. Kwa kuwa wao ni wengi, wengi wao wanaishi Kenya na inaonekana kwamba, zipo hisia tu kila Mjaluo anayeonekana Tanzania hapa anakuwa kama mhamiaji. Ni lini sasa hawa Wajaluo ambao ni raia wa Tanzania wanaoishi mpakani na hasa kwenye vijiji nilivyovitaja, ni lini watapewa haki yao ya msingi kama raia kuliko kusumbuliwa kila siku kuonekana kama wahamiaji wakati wao ni wa karibu hapa wanaishi maeneo ya Rorya?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; hivi mtu akiwa mlowezi, ni lini ulowezi wake unakoma? (Kicheko)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana babu yangu, Mheshimiwa Getere, kwa maswali mawili mazuri sana. Moja, hili alilosema la Wajaluo, si Wajaluo tu watu ambao wana makabila yanayoingiliana na nchi za jirani kupata misukosuko ya aina hiyo, yapo matatizo haya Mikoa yote ya pembezoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimwambie tu kuhusu lini hilo litakwisha ni kwamba, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani, kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa wako katika hatua za mwisho za kufanya utambuzi na badaye kuwapatia vitambulisho wananchi wote wa Tanzania. Kwa hiyo, pale watakapokuwa wameshapata vitambulisho hapatakuwepo na mtu tena kuhisiwa hisiwa kwa ajili ya makabila kuwa yana mwingiliano katika nchi za jirani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu walowezi na lenyewe liko karibu sana na hili nililolisema. Kuna taratibu za walowezi, watu waliolowea hapa kupewa uraia wao. Kwa hiyo, kwa wale ambao watakidhi vigezo na wakapewa uraia watapewa vitambulisho na hilo litakuwa limekoma la kuwa walowezi na watakuwa Raia wa Tanzania. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante kwa kuwa hili tatizo la uwepo wa ofisi mmbovu na ambazo hazina hadhi katika maeneo yetu ya Tanzania na zinatutia aibu limekuwepo kwa muda mrefu sasa nini commitment ya Serikali kwamba sasa hizi aibu tunaziondoa lini katika maeneo hayo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa mambo haya pia yanahusu mambo ya uhamiaji na kwa kuwa katika Jimbo la Rorya na Jimbo la Bunda kwenye vijiji vya Tlinati, Jabuzume na Nyaburundu kumekuwepo na hisia za kuwaita watu jamii ya Wanandi, Wakisii na Wajaruo kwamba ni wahamiaji na hasa wakati wa uchaguzi, je, ni lini sasa Serikali katika upande wa uhamiaji watamaliza hii kero ili wananchi waishi huru? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana na nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwani amekuwa mstari wa mbele sana kwenye kufuatilia mambo yanayohusu wananchi wake na mpaka kuna siku aliwahi kunipeleka kufanya mkutano saa mbili usiku, na kwa kweli wananchi wake hawakufanya makosa kumchagua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali hili analolisema kwamba lini Serikali itamaliza tatizo hili; sasa hivi Serikali iko kwenye uandikishaji wa Watanzania kupewa vitambulisho vya uraia na zoezi hili linaendelea mikoa yote, na Mkoa wa Mara ni moja ya mkoa ambao zoezi hilo limefanyaka vizuri sana. Pale ambapo zoezi la upatikanaji wa vitambulisho vya uraia vitakuwa vimepewa kwa kila Mtanzania tutakuwa tumemaliza tatizo la watu kuhisiana kuwa si raia kwa maslahi ya kiuchaguzi kama alivyosema ama kwa kutazamana kwenye sura ama lugha mtu anapoongea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo punde ambapo kila mmoja atakuwa na kitambulisho cha uraia tutakuwa tumelimaliza tatizo hilo na wananchi wake wataendela kukaa kwa usalama. (Makofi)
MHE. BONIFACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Wilaya ya Bunda ni moja ya wilaya zinazolima pamba sana kwa Mkoa wa Mara. Ginnery ya Buramba na Ushashi baada ya kilichokuwa Chama cha Ushirika cha Mkoa wa Mara kufa au kufilisika, zilikabidhiwa mufilisi. Ni lini sasa Waziri atafika kuangalia zile ginnery mbili ambazo zimekabidhiwa mufilisi muda mrefu na ziko taarifa kwamba mufilisi ameuza kila kitu na vile viwanda vimetelekezwa? Ni lini Waziri atafika pale kuangalia makabidhiano yaliyokuwepo ya Mara Corp na hali ilivyo kwa sasa kwa ginnery hizo mbili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya kumaliza Bunge. (Kicheko/Makofi)
MHE. BONIPHACE P. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza…
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ujenzi wa Vituo vya Afya katika nchi yetu kwa maeneo mbalimbali. Kuna vituo vimepata shilingi milioni 500 na kuna vituo vimepata shilingi milioni 400. Sasa huwa najiuliza na wanasema vituo vyote vimepata shilingi milioni 700; shilingi milioni 200 kwa vituo vilivyopata shilingi milioni 500 inaenda MSD na shilingi milioni 300 kwa vituo vilivyopata shilingi milioni 400 imeenda MSD. Sasa huwa najiuliza…
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii tofauti ya fedha za kwenda kununua vifaa MSD ya shilingi milioni 300 na shilingi milioni 200 na shirika ni lile lile, la Serikali tofauti yake inatokana na nini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili linajirudia kwa mara nyingine na nikiwa hapa niliwahi kutoa ufafanuzi kwamba kwanza inategemeana na source of fund; kuna maeneo mbalimbali ambayo tumepata fedha.
Kwa hiyo, inategemea shilingi milioni 500 au shilingi milioni 400, kama ni Benki ya Dunia, Canada, Serikali ya Tanzania lakini pia inategemeana na hali ya Kituo cha Afya husika kwa sababu kuna baadhi ya Vituo vya Afya vinahitaji ukarabati mdogo, vingine ukarabati wake ni mkubwa. Kwa hiyo, tumekuwa tukifanya scope kujua uhalisia ili Kituo cha Afya kiweze kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala zima la pesa ambazo zinapelekwa MSD, majibu yake hayana tofauti sana na hili jibu la mwanzo kwa sababu ukienda Kituo cha Afya Manyamanyama ambacho labda kina x–ray center haiwezi kuwa sawa na kituo cha afya kingine ambacho hakina mashine kama hiyo.
Kwa hiyo, Serikali tumekuwa tukiyazingatia hayo wakati tunapeleka fedha, ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini pia nawapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake na watendaji wote wa Kilimo, wanajitahidi sana kuokoa zao la pamba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Kabla sijauliza, nisahihishe tu kwenye Hansard kwamba hakuna Jimbo linaitwa Bunda Vijijini. Kuna Jimbo linaitwa Bunda. Kwa hiyo kwenye Hansard kusomeke kuna Jimbo linaitwa Bunda.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa wakulima wa pamba na kwa kuwa katika jibu la msingi Naibu Waziri amesema kuna watu walikopa pamba na kuna vikundi vilifanya mkataba na wana makampuni kukopa pamba, sasa hili tamko la Serikali la kukata shilingi moja kwa kila mkulima ili kulipia pembejeo na hata yule ambaye hakukopa, ni la nini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali imejiandaa vipi sasa kukabiliana na changamoto zitakazojitokeza kutokana na miongozo yake ya mara kwa mara ambayo haijawa na maandalizi? Kwa mfano, kuna suala la wakulima kufungua akaunti, kuna suala la pamba kununuliwa na ushirika au na watu binafsi kwa maana ya ushirika kununua pamba, kuna suala la kwamba ushirika hauna fedha ya kununulia pamba, sijui ni watu binafsi watatoa kwenye ushirika; Serikali imejiandaa vipi sasa kukabiliana na matatizo haya ambayo watu watayapata kutokana na miongozo yake hii mifupi? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya swali la msingi. Pia nampongeza Mheshimiwa Getere kwa maswali haya ya muhimu sana katika tasnia ya pamba. Nianze na swali lake la nyongeza la kwanza kuhusu fedha; shilingi moja moja aliyoisema.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pembejeo waliyopata wakulima wengi walio katika mkataba ni lazima ilejeshwe na utaratibu wa kuirejesha ile pesa ni kwa makato kutokana na mauzo yao. Hiyo fedha inayokatwa siyo tu kwamba itafanya kazi ya kurejesha pembejeo waliyopata, lakini ili twende vizuri katika msimu ujao tunapaswa kuwa na fedha ya kuanzia kwa ajili ya kupata pembejeo hizo hizo ambazo wakulima watapata. Ndiyo maana Serikali imeshatamka kwamba msimu ujao wakulima wa pamba kote nchini hawatakopeshwa au pembejeo kwa maana ya dawa au mbegu za pamba. Watapata bure na hii inatokana na hii fedha ambayo wanakatwa sasa hivi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la nyongeza, siyo kwamba Serikali imesema ushirika utanunua pamba ya wakulima, kwa sababu wakulima wenyewe ndiyo ushirika. Kwa hiyo, kitakachofanya sasa hivi na kinachofanyika ni ushirika unakusanya pamba ya wanachama wake halafu wanunuzi wanaenda kununua kwenye ushirika huo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, makampuni kama alivyosema Naibu Waziri yanafanya biashara lakini kuna maeneo ambayo yana mahitaji makubwa na biashara ipo lakini hayajawahi kupata huduma za mawasiliano kwa muda mrefu. Naomba kujua ni lini Vijiji vya Nyangere, Nyaburundu, Nyabuzume, Tiling’ati, Tingilima na Kibara Ginnery zipata mawasiliano? Kwa mfano Kibara Ginnery ina kiwanda muda mrefu lakini hakuna mawasiliano, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Getere na nimpongeze kwa jinsi ambavyo anafuatilia sana suala la mawasiliano hasa kwenye hii Kibara Ginnery. Vilevile nimshukuru kwamba ni mmoja kati ya Wabunge ambao wameleta maombi yao ofisini kwangu kwa ajili ya kwenda kuwekewa minara kwenye maeneo yote ambayo hayana mawasiliano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niamuahidi kama nilivyozungumza wakati najibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sakaya kwamba baada ya Bunge hili nitafanya ziara karibu nchi nzima, specifically kwa wale Waheshimiwa Wabunge wote ambao wameleta barua ofisini kuomba mawasiliano. Nitafanya ziara, tutaanisha maeneo, tutatangaza tenda kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, tutafungua tenda kabla ya mwezi Oktoba, minara itaanza kujengwa maeneo mbalimbali. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Nadhani sasa umefika wakati kwa Serikali kuamua kuangalia haya mambo ya majengo ya Mahakama kwa sababu duniani kote haki ndiyo inajaaliwa, lakini kumekuwa tu na mazoea ya kujibu kwa sababu nimemuona Mheshimiwa Lameck Airo akiwa na hoja hii miaka mitatu iliyopita na ni miaka 11 sasa toka Wilaya hii ianzishwe. Sasa uhakika ni upi? Kila mwaka anauliza wanasema mwaka unaofuata, kila mwaka anauliza anaambiwa mwaka unaofuata. Sasa Waziri atuthibitishie kwamba ni kweli bajeti inayokuja hiyo Mahakama itajengwa kwa Wilaya ya Rorya.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Jimbo la Bunda kuna Mahakama ya Nyamswa, imekuwepo muda mrefu sana hiyo Mahakama ilijengwa na Mtemi Makongoro miaka hiyo mpaka leo, ni lini sasa Serikali itaenda kukarabati ile Mahakama na kuifanya iwe ya kisasa kwa ajili ya kusaidia watu wa Jimbo la Bunda? (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimhakikishie Mbunge aliyeuliza swali kwamba Mahakama hiyo itajengwa katika mwaka huo wa 2019/2020 na siyo Mahakama hiyo tu bali Mahakama zote ambazo zimepangwa kujengwa katika mwaka huo kwa Mkoa wa Arusha ikiwa ni Arumeru na Ngorongoro; kwa Mkoa wa Dodoma ikiwa Bahi; kwa Mkoa wa Geita ikiwa Geita; kwa Mkoa wa Kagera ikiwa ni Muleba, Bukoba, Ngara, kwa Mkoa wa katavi ikiwa ni Mpanda na Tanganyika; na kwa Mkoa wa Kigoma ikiwa ni Uvinza na Buhigwe.
Vile vile kwa Mkoa wa Kilimanjaro ikiwa ni Same; kwa Mkoa wa Lindi ikiwa ni Nachingwea; kwa Mkoa wa Manyara, Babati, Hanang’, kwa Mkoa wa Mara ni Rorya na Butiama; kwa Mkoa wa Mbeya itakuwa Rungwe; kwa Mkoa wa Morogoro Gairo, Mvomero, Morogoro, Malinyi; kwa Mkoa wa Mtwara, Newala, Mtwara, Tandahimba; kwa Mkoa wa Mwanza, Kwimba; zote hizo ni Mahakama ambazo zitajengwa kwa mwaka wa fedha 2019/2020 na fedha yake inatokana na mkopo kutoka Benki ya Dunia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo vyanzo vya fedha vipo na bado zipo Wilaya nyingine nyingi ambazo Mahakama zitajengwa mwaka huu wa 2019/2020. Kwa hiyo ningependa nimhakikishie hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Mahakama ya Nyamswa, kabla ya Bunge hili kuanza nilifanya ziara ya Mkoa wa Mara na mahali ambapo nilipita pia ni Nyamswa. Hili ni jengo la zamani ambalo linahitaji kukarabatiwa na hilo litatafutiwa fedha katika mpango wa dharura, itakapopatikana ili Mahakama hiyo ya Nyamswa iweze kukarabatiwa. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, niwapongeze Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kunipa gari la kusaidia kufukuza wanyama waharibifu kwenye maeneo yangu, lakini pia, najua wana mpango wa kupeleka fedha za kifuta jasho katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa, sasa ni miaka 15 Vijiji vya Hunyali, Kihumbu, Maliwanda, Salakwa, Kyandege, Tingilima, wamekuwa ni wahanga wakuu wa wanyama waharibifu wa mazao, sasa Serikali ina mpango gani sasa mbadala ikiwepo kupima vijiji hivyo ili kupata Hati Miliki za Kimila na kuendesha maisha ya wananchi wa makazi hayo?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa sasa kuona ni kuamini na kuamini ni kuona, ni lini sasa Wizara au Waziri atatembelea maeneo haya, ili kujihakikishia hali halisi ya uharibifu huo? Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, kwanza ni kweli kabisa kwamba, sasa hivi Wizara ina mpango mkubwa mahususi wa kuhakikisha kwamba vijiji vyote ambavyo vinazungukwa na Hifadhi za Taifa vinakuwa na mpango bora wa matumizi ya ardhi. Hili tunalifanya kuanzia mwaka wa fedha unaoanza Julai mwaka huu. Katika kutekeleza hilo tunashirikiana na Wizara ya Ardhi, ambapo ndiyo wamepewa hizi fedha kwa ajili kusaidia kupima vijiji vyote hivi ili wawe na mpango mzuri na kuhakikisha matumizi yanaeleweka vizuri kabisa.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, kuhusu kwenda kutembelea na kujionea hali halisi, naomba nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tuko tayari wakati wowote mara baada ya Mkutano huu wa Bunge kumalizika tutapanga ni lini tunaweza kufika kule ili tujionee hali halisi ilivyo huko.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kabla ya kuuliza swali, naomba kuipongeza Wizara ya Kilimo, Bodi ya Wakurugenzi wa Pamba kwa kuwapa nafuu wakulima wa pamba kwa kuwapa utaratibu mzuri wa ununuzi wa pamba na kuwaondolea kero ambayo ilikuwa inawapa usumbufu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, barabara ya Mgeta – Mihingo – Nikomalile na Sirolisimba imekuwa na ahadi ya muda mrefu na imeharibika sana na ina umuhimu mkubwa wa kuleta wateja katika Mnada mkubwa wa Mgeta ambao unafanyika mara mbili. Je, ni lini barabara hii itakamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA):
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nimpongeze sana Mheshimiwa Getere kwa sababu mimi kila nikikutana naye namuita mzee wa Silolisimba kwa sababu yah ii barabara ya Mgeta – Silolisimba, anaifuatilia kweli. Kwa kweli kama nilivyokuwa nimemuahidi ilikuwa ni kuhakikisha kwamba barabara hii tunaipa kipaumbele kwa sababu ina matatizo makubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimfahamishe tu Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Bunda kwa ujumla kwamba baada ya mvua kuwa zimepungua mkandarasi yuko site na nikuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge mazungumzo ambayo tumeyafanya na kuhakikisha kwamba barabara inatengenezwa majibu yake yanapatikana kwa sababu fedha za kupeleka kwa ajili ya barabara hii zimeshapatikana, kati ya wiki hii na wiki ijayo fedha zitakwenda. Nimuombe na kumuagiza tu mkandarasi aliyeko site afanye kazi kwa nguvu na mimi baada ya Bunge hili ntafika kuona kwamba kazi inaendelea ili kuweza kuondoa hii shida ambayo ipo katika eneo hilo. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Getere, tuendelee kushirikiana na kubadilishana mawazo lakini nia yetu ni moja ni kuhakikisha kwamba tunaboresha miundombinu hii ya barabara. (Makofi)
MHE. BONIPHANCE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Vituo vya polisi vya Nyamuswa, Mgeta vimejengwa miaka ya 60, majengo yake sasa hivi ni hatarishi na wananchi wako tayari kusaidiana na Serikali kujenga vituo vile kwa kutoa nguvu kazi ya tofali, maji, kokoto na mawe. Je, Serikali iko tayari kushirikiana na wananchi kujenga vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Getere kwa jitihada zake za kuhamasisha wananchi kuweza kupata vifaa ambavyo amevizungumza kwa ajili ya ujenzi wa vituo. Nataka nimhakikishie kwamba, Serikali itahakikisha kwamba tunaunga mkono jitihada hizo ili kuweza kufanikisha malengo ambayo wameyakusudia.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Diwani wa Kata ya Mihingo Mheshimiwa Nyambula Nyamhanga yuko lockup miezi sita sasa kwa kosa la uchochezi. Naomba kupata ufafanuzi wa Serikali, ni njia gani tuitumie huyu Diwani apate dhamana, kwa hiyo kesi ya uchochezi kwa sababu ana miezi sita yuko gerezani bila kupata dhamana? (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu jambo alilolisemea Mheshimiwa Mbunge ni mahsusi na kwa mujibu wa sheria kuna makosa yenye dhamana na kuna makosa yasiyo na dhamana; nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge tuje tuliongee. Pia nimpongeze kwa kufuatilia sana masuala ya wapiga kura wake. Kama ni jambo ambalo lina dhamana maana yake taratibu tu za dhamana zitafuata ili ziweze kukamilika na Mheshimiwa Diwani aweze kupata dhamana. Mara zote yale makosa yasiyo na … (Makofi)
MHE. BONIPHANCE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Wakati fulani hili Bunge haya majibu tunayopewa tuwe tunayachunguza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 12 ambayo wameisema hapa, ni kweli kulitokea vurugu na mimi kama kiongozi, Mbunge nilipiga simu saa 12.00 asubuhi kwa Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya kuwataarifu kwamba kuna vijiji viwili vinagombania ardhi na kuna watu wameenda kulima, akina mama wawili wakanyang’anywa ng’ombe kwa upande wa pili, tulivyokuwa tumepewa taarifa hizo. Saa 12.00 asubuhi viongozi wote wa Mkoa na Wilaya wakasema wamepokea taarifa, Jeshi la Polisi limekwenda pale saa 11.00 jioni watu wamepigana mpaka wameuana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi msako uliofanyika saa 11.00 jioni, tarehe 13 tulienda pale viongozi wote, Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa na vyombo vya habari vilikuwepo, maduka yote yamechukuliwa. Mambo mengine kusema hapa ni aibu, nachokiomba Serikali katika hili …
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu Serikali katika hili waende wakaangalie hiyo halisi ilivyokuwa na sisi tuna ushahidi wa kutosha juu ya jambo hilo. Hilo swali la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa chanzo cha mgogoro huo ni mgogoro wa ardhi ambao una vijiji vitatu ambapo kimsingi mgogoro ule ni kama umeisha. Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa aliyekuwepo Mheshimiwa Simbachawene alishafika pale akatoa maamuzi, maeneo yale yamegawanywa na vigingi vimewekwa. Ni lini sasa, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa itaenda kuweka GN kwenye maeneo hayo ili kumaliza mgogoro huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba uniruhusu nimsifu sana Mheshimiwa Boniphance Mwita Getere. Eneo analoliongoza lina changamoto nyingi sana hususani hizi za kiulinzi na kiusalama. (Makofi)
Mheshimiwa Mweyekiti, ombi lake aliloliomba, kwa sababu uchunguzi wa kipolisi bado unaendelea, haujakamilishwa kabisa, napenda nimhakikishie kwamba uchunguzi ule utaendelea kufanyika kwa kufuata taratibu za sheria za Polisi na sisi kupitia Kamati zetu za Ulinzi na Usalama, Mkoa na Wilaya tutafanya tathmini ya kina kuangalia matatizo gani yalijitokeza ili tuweze kuyatatua tukishirikiana naye.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili, uwekaji wa GN kuondoa migogoro iliyokuwepo kwenye vijiji husika, naomba sana Mheshimiwa Mbunge awe na subira, suala hili linafanyiwa kazi kwa ujumla kwa nchi nzima. Tulikuwa na migogoro zaidi ya 366 katika nchi nzima na tunaifanyia kazi kwa pamoja. Kwa hiyo, kuweka usuluhisho wa aina hiyo kwenye eneo moja tu la nchi, tunaomba sana Mheshimiwa Mbunge awe na subira tunalifanyia kazi kwa nchi nzima. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, nimshukuru kwanza Naibu Waziri kwa majibu mazuri sana, lakini kwa ujumla niwashukuru watu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Waziri na viongozi wake wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hili la wanyama waharibifu, hasa tembo, katika Jimbo la Bunda na kwa kata tatu ambazo zina vijiji 18 ni kubwa sana. Nikiangalia toka tuanze kulipa haya malipo ya fidia, ni mabilioni ya hela yanaenda na nimeona hapa tumekuwa na mikakati mingi, kuweka ukuta, kuweka pilipili na kuchimba mitaro na wengine huko vijijini kwenye Jimbo la Bunda wanasema tembo hawa hawana uzazi wa mpango, mnasema tembo wamepungua lakini ni wengi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuuliza, ni lini sasa mikakati halisi ya Serikali itakuwepo ya kuzuia mnyama tembo ili kutoleta umaskini kwenye maeneo ya kwetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba katika eneo la Serengeti, na hasa katika Jimbo la Bunda kumekuwa na matatizo hayo na changamoto hizo ambazo zimekuwa zikijitokeza. Suala ni lini hasa tutakuja na mipango, sasa hivi tunakuja na mpango mkakati ambao tutausema tutakapokuwa tunawasilisha bajeti yetu ya mwaka 2018/2019, ni hatua gani ambazo tunategemea kuchukua katika maeneo mbalimbali ya Hifadhi za Taifa na maeneo mengine ya mapori ya akiba ili kukabiliana na changamoto hizi za wanyama waharibifu.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge naomba tu aendelee kutusubiri, pale tutakapowasilisha bajeti yetu basi atuunge mkono ilia one hizo hatua ambazo tunakwenda kuchukua ambazo ndizo zitakazokuwa suluhu ya changamoto mbalimbali.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, nimshukuru kwanza Naibu Waziri wa Kilimo, Ndugu yangu Bashungwa kwa uadilifu wako, nadhani Mungu atakusaidia utafika unakoenda. Napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza la kwanza, na hili niliseme wazi kwa Waziri aliyopo na wewe mwenyewe, na kwa Wabunge wote nadhani unalijua hili, tatizo kubwa la pamba ni mambo mawili tu, la kwanza ni bei ya pamba, la pili ni usambazaji wa pembejeo kwa wakati ambao haufai.

Mheshimiwa Spika, suala la bei, naomba kujua kupata ufafanuzi, ni kwa nini sasa Serikali isitafute masoko ya ndani na masoko ya nje kwa wakati muafaka kwa msimu unaofaa, ili Wakulima wa pamba wapate bei nzuri ya kutosha?

Swali la pili kwa kuwa mwaka jana kwa msimu 2018/ 2019 Serikali ilikuja hapa Bungeni ikatuomba wakate shilingi mia kwa kilo ya pamba kwa wakulima, na lengo lilikuwa kupunguza au kufuta kabisa kero ya usambazaji wa mbegu za pamba au madawa kwa wakati muafaka, nini kimetokea mpaka leo Wakulima wa pamba wanateseka na mbegu hazipatikani kwa wakati na madawa hayapatikani kwa wakati, nini tatizo,? Tatizo ni ubovu wa bodi ya pamba? au ni mikakati mibovu ya Wizara ya Kilimo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA): Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Boniphace Getere kwa namna anavyohangaikia changamoto za Wakulima Jimboni kwake Bunda hususani zao la pamba.

Mheshimiwa Spika, tatizo la bei na usambazaji tayari Serikali chini ya mfumo wa ushirika tunaendelea kuimarisha ushirika ili ushirika uweze kuwajibika kwa Mkulima kwa kuhakikisha Mkulima anapata pembejeo kwa wakati anazingatia ubora na tayari Wizara yetu kwa kushirikiana na Taasisi zilizopo chini ya Wizara tunaendelea kutoa elimu ili wakulima wetu wa pamba wazingatie kupanda kwa kutumia kamba ambayo ina vipimo.

Mheshimiwa Spika, pia, sambasamba na hilo usambazaji wa pembejeo hususani viuatilifu kwa misimu iliyopita vilikuwa vikichelewa lakini tayari Wizara tumeshakaa na kuhakikisha tuna mkakati wa kuhakikisha msimu huu viuatilifu vina wafikia wakulima wetu kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la Mheshimiwa Getere ni kuhusu masoko ya ndani na nje nimuhakikishie Mheshimiwa Getere kwa vile ni mfuatiliaji mzuri tutakaa naye pamoja na Waheshimiwa Wabunge wanaotoka Mikoa inayolima pamba na kuhakikisha tunakuwa tuna mfumo mzuri ambao utamuhakikishia mkulima kupata bei nzuri lakini na shilingi mia moja ambayo wanakatwa tutaangalia namna ya kuangalia mfumo mzuri ili makato ya mkulima yamsaidie katika kuwa na Kilimo cha tija, ili aweze kupata pato zuri katika msimu wa kuuza pamba, nashukuru.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeze tu Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali kwa jinsi wanavyoshughulikia suala hili katika Mgodi ule wa ACACIA Nyamongo kule. Nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tatizo la fidia katika eneo la Nyamongo limekuwa la muda mrefu; na ni miaka mingi kila siku watu wanadai na wengine wanadai malipo hewa na wengine malipo halali: Ni lini sasa Serikali itamaliza hili tatizo kwa muda muafaka ili kutufa kabisa tatizo la kudai madai ya Nyamongo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, matatizo yanayotokea Nyamongo, yanafanana sana na matatizo yanayotokea katika kijiji changu cha Nyabuzume Jimbo la Bunda Kata ya Nyamang’uta; na kwa bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri wewe ulifika kenye kile kijiji, kuna wachimbaji wako pale, wanapiga yowe za muda mrefu, wanasumbua wananchi na hawawezi kushirikiana nao katika kupeana zile kazi za kijiji; nawe uliahidi kumaliza hilo tatizo. Ni lini tatizo la Nyabuzume wale wachimbaji wasio halali au walio halali ambao hawatekelezi suala la kuondoa matatizo ya wanakijiji katika kijiji kile?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa madai ya Nyamongo kule North Mara katika ile kampuni ya Acacia yamechukua muda mrefu. Yamechukua muda mrefu kwa sababu mbili. Sababu ya kwanza ni kampuni yenyewe ya Acacia ilichelewa kulipa malipo kwa muda uliostahili. Sababu ya pili ni kwa wananchi wenyewe ambao baada ya evaluation ya kwanza ku-expire, evaluation ya pili kuna watu walifanya speculation, yaani walifanya kutegesha, kwa maana waliongeza majengo, wakaongeza mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli limetupa shida sana suala hili kwa sababu evaluation ya mwanzo ilikuwa inaonekana ni ndogo, kuja kufanya evaluation ya pili imeonekana ni kubwa sana. Mfano kuna sehemu ya Nyabichele. Wao walithaminishiwa kwenye mazao yao; gharama ilikuwa ni shilingi bilioni 1.6, lakini baada ya evaluation ya pili kuja kufanyika, gharama yake ikaonekana ni shilingi bilioni 12. Hili limefanya kampuni kusita kuweza kulipa fedha hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yangu ya msingi nilisema kwamba hili suala lipo kwa Chief Valuer na leo nimeongea na Chief Valuer amefanya evaluation na ameandika barua kwa North Mara kwa maana ya Kampuni ya Acacia, ile evaluation ambayo wameandikiwa na Chief Valuer wailipe immediately. Wailipe mara moja, wasipoteze
muda ili kuondoa manung’uniko. Vilevile kupitia Serikali ya Mkoa wa Mara, tumeelewana na Kampuni ya Acacia kwa maana ya North Mara, walipe fidia kwa wale wananchi wanaodai wanaona kabisa kwamba wananchi hawa wana madai yao ya haki, hawana dispute yoyote, hawana mgogoro wowote, hao walipwe mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna wananchi wengine ambao ni 138 toka mwaka 2016 kuna cheque ya thamani ya shilingi bilioni 3.2 wamegoma kwenda kuchukua kwa sababu wanalishana maneno, wanasema kwamba wanacholipwa ni kidogo. Nawaasa na ninawaomba, wananchi ambao cheque zao ziko tayari, waende wakachukue cheque zao mara moja ndani ya wiki hii. Wasipochukua ina maana sasa Serikali ya Mkoa itachukua hatua nyingine na itakuwa vinginevyo. Kwa hiyo, itazidi kuwacheleweshea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nawaomba wananchi wa Mkoa wa Mara na maeneo ya North Mara tusilishane maneno. Watu ambao wana haki, wanatakiwa kulipwa na cheque zao ziko kihalali, waende wakachukue cheque zao mara moja. Kampuni ya North Mara, ndani ya wiki hii tumeshawaambia, yale maeneo ambayo hakuna dispute, walipe mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuhusiana na suala la Bunda kule ambako Mheshimiwa Mbunge amelielezea, kwa wale watu wanaomiliki PLs na hawazitumii, nimezungumza hapa hata jana, kwamba kwa wamiliki wa PLs wasiozitumia, hawafanyi tafiti, sisi tunapitia PL moja baada ya nyingine. Tunakwenda kufuta hizo PL na tunakwenda kuwapa wachimbaji wadogo wachimbe ili waweze kujipatia kipato na Serikali iweze kupata mapato kupitia uchimbaji mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza, niwashukuru sana Wizara ya Ujenzi kwa kunipa fedha za kutengeneza barabara ya Mugeta Siloli Simba. Na kwa kuwa ile barabara ilikuwa na km 21 na zimetengenezwa kilomita fulani na zimebaki kilomita tisa. Naomba kujua kutoka kwa Waziri ni lini sasa watapeleka fedha ili kumalizia kilomita tisa zilizobaki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa
Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tumefanya ujenzi wa kuboresha sehemu ya barabara ya Mugeta kwenda Siloli Simba, lakini Mheshimiwa Mbunge atakubaliana name kwamba sehemu ya kilomita 11 iliyojengwa, barabara haikuwepo kabisa, lakini kile kiwango cha barabara kimewavutia Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa eneo hili ili sehemu ambayo ilikuwa na barabara awali na yenyewe ifanyiwe maboresho. Kadri tunavyopata fedha kilomita hizi chache zilizobaki tunafanya maboresho.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mpaka wa hifadhi wa Guruneti na Mto Rubana katika Vijiji vya Hunyali, Mariwanda, Kihumbu, Sarakwa na Mgeta lakini limekuwa tatizo la buffer zone inayotoka kwenye mto kuelekea vijijini na kuzuia watu kwenda kunywesha ng’ombe na malisho kwenye maeneo haya. Mheshimiwa Waziri alishatoa maelekezo ya mdomo lakini ni lini Serikali itapeleka sasa vigezo vya kisheria vya kuondoa eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli kwamba kutokana na matatizo ya mwingiliano wa shughuli za kibinadamu na wananchi na hifadhi pamekuwepo na migogoro mingi ambayo sasa hivi kama ambavyo nimekuwa nikijibu maswali yangu mengi Serikali inayafanyia kazi. Nimkumbushe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba suala lake tumekwishalizungumza, tunasubiri maelekezo ya Kamati ambayo iliundwa na Mheshimiwa Rais itakapotoa maelekezo tutatengeneza buffer zone ambayo itaruhusu wafugaji kwenda kwenye mto kunywesha mifugo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Meshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, lakini niipongeze Wizara ya Nishati, Waziri wake Mheshimiwa Dkt. Kalemani na Mheshimiwa Subira, Naibu Waziri na Watendaji wake wote kwa kasi ambayo wanaionesha sasa kwenye Jimbo la Bunda. Natambua kuna Vijiji vya Nyabuzume, Tiring’ati, Bigegu, Nyaburundu, Mihingo, Rakana, Manchimweru, Nyang’aranga, Sarakwa na Tingirima, wameweka nguzo za umeme. Swali langu la kwanza hapa, ni lini sasa umeme utawaka kwenye maeneo haya kwa sababu ninapouliza swali hili sasa hivi hapa kuna akinamama zaidi ya 100 wanataka kusikiliza wamechoka na mambo ya vibatari kwenye maeneo yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kuna maeneo ya Nyamatutu, Saba-Osanza, Mmagunga, Nyamakumbo, Sanzate, Nyansirori, Saloka-Guta, Nyamuswa A. Mheshimiwa Waziri rafiki yangu Dkt. Kalemani, kutoa transfoma nane kwenye maeneo ya taasisi kama vituo vya afya, shule za msingi, sekondari survey ilishafanywa na Serikali imetumia hela pale tangu 2016, ni lini sasa zile Taasisi zitapata umeme, kuweka transfoma nane shida iko wapi?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri alivyojibu majibu mazuri kwenye swali la Mheshimiwa Mbunge Getere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge Getere anavyofuatilia masuala ya umeme katika Jimbo la Bunda Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napenda nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza amependa kujua ni lini sasa vijiji vya Bunda ambavyo vinapelekewa umeme vitapata umeme. Kwanza nianze kusema hapa tunapoongea wakandarasi wako site na hivi sasa vijiji takriban 11 wameshavifanyia kazi. Leo na jana wakandarasi wako site, Derm Electric, wanafanya kazi katika Vijiji vya Mwanchimweru, Nyanharanga, Mahanga, Lakani pamoja na Tingirima ambapo vyote watawasha umeme katika wiki inayokuja. Katika Jimbo la Mheshimiwa Getere vimebaki vijiji vitano tu vya Sarakwa, Nyabuzume, Tingirigi pamoja na vijiji anavyovitaja vitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala lake la pili ambalo ni la msingi kabisa, maeneo ya vijiji takribani 11 yana umeme na vitongoji vyake vina umeme shida ni shule za sekondari na zahanati ambazo hazijapata umeme. Nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge wakandarasi wameshaweka design, tuna mpango wa kuongeza umeme katika vitongoji unaoanza mwezi ujao. Kwa hiyo, maeneo yote ya Shule za Msingi za Nyamatutu, Saba Osama, Nyamakumbu, Maguga, Salokikwa pamoja na Musa na Makongolai A&B vitapelekewa umeme pamoja na taasisi zake.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa niwashukuru Wizara ya Maji kwa sasa kwa kweli tuseme ukweli kwamba, viongozi wote Mawaziri, Makatibu na watendaji wote sasa wako kazini, wanafanya kazi vizuri, niwashukuru sana. Katika Jimbo la Bunda wataalam walifanya tathmini ya kuchimba visima vya maji ikaonekana kwamba, visima vinakauka, Wizara ikaja na mkakati wa kuchimba malambo zaidi ya malambo 16 ambayo ni matumizi ya maji, sasa kwa mwaka huu wamechagua kuchimba malambo matano. Nilitaka kuuliza tu Waziri, ni lini sasa haya malambo matano yatafanyiwa kazi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kiukweli anafanya kazi kubwa sana. Jana tu tulikuwepo nae katika Wizara yetu ya maji na Katibu Mkuu na moja ya makubaliano ni katika kuhakikisha tunatia fedha kwa ajili ya uchimbaji wa mabwawa zaidi ya matano. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nataka nikuhakikishie sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa Wananchi wako wa Bunda Vijijini kuweza kuchimbiwa mabwawa haya na waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, pia, nitumie nafasi hii kuwapongeza Wabunge wa Mkoa wa Mara wanaotokana na Chama cha Mapinduzi kwa mshikamano wao na kuweza kupigana. Zaidi ya miradi Mgango, Kyabakari tumekwishasaini, lakini tunakwenda kutatua tatizo la maji Mugumu pamoja na Tarime. Ahsante sana.
MHE. BONIFACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Katika Jimbo la Bunda Vijijini kuna Mradi wa Maji Nyamuswa na kuna Mradi wa Maji Mgeta na Naibu Waziri ailifika kwenye maeneo hayo lakini mpaka sasa ile Kamati aliyoiunda kufuatilia shughuli hizo haijakwenda vizuri.

Je, Naibu Waziri yuko tayari sasa kushughulika na hilo jambo ili watu wa Nyamuswa na Mradi wa Mgeta-Nyangarangu wapate maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nipo tayari. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali ambayo yametolewa na Naibu Waziri, lakini mimi shida yangu ni moja tu. Mimi sio Mhasibu sana lakini ukitazama ukweli uliopo ni kwamba ukaguzi huu ambao ni wa Kimataifa unaonyesha nyaraka za kihesabu na vitabu vya kihesabu vinavyokaguliwa kama viko sawa, lakini havionyeshi matumizi ya ndani kama shirika limepata hati safi kwa maana kwamba halina ubadhirifu. Sasa je, Serikali inaonaje sasa, utaratibu wa Kimataifa uendelee lakini tuwe na utaratibu wa ndani ili kutambua ubadhirifu unaotokea kwenye mashirika yaliyo na hati safi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba kuna dhana ya ukaguzi ambapo wanaona kama kuna matatizo makubwa yanatokea kwenye athari za kihesabu; sasa haya matatizo makubwa na haya madogo anayoyataja sijayaona kwenye majibu yake; pengine angeweza kutusaidia kwamba haya matatizo makubwa ya kiathari za hesabu ni yapi kwenye shughuli za kimahesabu?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nayajibu maswali yake yote mawili kwa sababu yote jibu lake ni moja. Zipo aina tofauti za kaguzi zinazofanyika ukiacha kaguzi za mahesabu kama nilivyosema ili kujibu maswali yake yote mawili kwamba ni matatizo gani makubwa na madogo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kunapokuwa na matatizo hayo mengine ambayo yako nje ya taarifa za kihasibu, huwa kuna ukaguzi wa ufanisi (performance audit) ili kuweza kuijuza Serikali juu ya namna bora ya kutumia rasilimali zake katika kubana matumizi; pia kuhimiza taasisi za Umma kuboresha utendaji wake wa kazi kufikia malengo kwa tija na kupata thamani halisi ya fedha.

Kwa hiyo, hapa tunakwenda kwenye miradi yenyewe kuangalia mchakato mzima wa mradi ulifanyikaje na mradi je, unajibu hali halisi ya thamani ya fedha kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna aina ya pili ya ukaguzi ambayo ni ukaguzi maalum (special audit). Ukaguzi huu maalum huombwa maalum na mtu specific au taasisi yenyewe ikiwa imegundua kuna matatizo hata kama taasisi yake ina hati inayoridhisha. Kwa hiyo, hii inakuwa na hadidu za rejea ambazo zimetolewa na mtu aliyeona kuna matatizo kwenye taasisi hiyo kwa hiyo inafanyika special audit ili kujibu hayo matatizo yaliyoonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna ukaguzi wa kiuchunguzi (forensic audit). Huu ni ukaguzi wa kisayansi ambao nao unakuwa na hadidu za rejea, tunakwenda zaidi ya special audit kujua matatizo haya yamesababishwa na nini kwenye taasisi husika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tuendelee kuziamini ofisi zetu na hasa Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa sababu wanafanya kazi zao kitaalamu zaidi.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi ya kuuliza swali dogo la nyongeza;

Mheshimiwa Mwenyekiti, msimu wa mwaka jana wa Pamba 2018/2019 tuliwaambia wakulima wa Pamba tuchange shilingi 100 kwa kila mkulima, iwe umekopa au hukukopa kwa maelezo kwamba msimu 2019/2020 hatukatwa pembejeo. Naomba kupata maelezo ya Serikali mwaka huu pembejeo wakulima wanakatwa au hawakatwi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwamba wakulima wanakatwa ama hawakatwi ni kwamba wakulima wanakatwa pembejeo za pamba msimu huu. Kilichotokea msimu uliopita fedha walizokatwa zililipa madeni ya pembejeo ambayo wakulima walipewa msimu uliotangulia, kwa hiyo msimu huu wakulima wa Pamba watakatwa pembejeo ambazo wamehudumiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezeee hapa na niseme na hili jambo liwe wazi, mfumo wa usambazaji pembejeo katika msimu ujao wa Pamba utabadilika. Tathmini ya awali iliyoonekana ni kwamba wakulima wa Pamba mwaka huu wanalipia pembejeo ambazo either hawakuzitumia ama wanabebeshwa mzigo, Wizara sasa hizi task force yetu iko kupitia mchakato mzima na tutachukua hatua kwa watu wote waliowaibia wakulima wa Pamba mwaka huu. Msimu ujao tunachokifanya mkulima wa Pamba Tanzania Cotton Board itatoa fomu ambayo itakuwa na duplicate ya fomu tatu, fomu moja ataachiwa mkulima aliyechukua pembejeo na itaonesha bei na thamani halisi, fomu nyingine itabaki kwenye AMCOS, fomu nyingine itabaki kwenye Ushirika ili msimu unapokuja wakati wa kuuza pamba gharama zake ziweze kuthibitishwa kabisa halali, kwa sababu sasa hivi kuna maeneo AMCOS na Ushirika unawaibia wakulima wa pamba ambao hawakuweza kubebeshwa gharama hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni kwamba wataendelea kulipa na tutabadilisha mfumo wa utoaji. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Namshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Amejieleza vizuri, tumeyaona kwenye karatasi hapo na yapo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, idadi ya watu katika nchi yetu inaongezeka na toka tumepata uhuru mwaka 1961 na Muungano 1964 tumeendelea kupambana na maadui watatu ambao ni ujinga, maradhi na umasikini. Angalau haya mawili ya maradhi na ujinga tunaelekea kuyamudu ndiyo maana idadi ya watu inaongezeka.

MWENYEKITI: Swali, swali!

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali; Serikali ina mpango gani sasa wa kupambana na adui namba moja ambaye ni umasikini unaoongezeka katika maeneo mengi hasa maeneo ya vijijini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kumekuwa na makundi makubwa ya vijana wanaohitimu elimu hasa Elimu ya Vyuo Vikuu. Sasa ndhi yetu ipo kwenye mkakati wa kujenga viwanda: Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwekeza katika viwanda vya Labor Intensive badala ya Capital Intensive ili kukidhi makundi makubwa ya vijana yanayohitimu shule na kwa sababu fursa tunazo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba umasikini ndani ya nchi yetu hauongezeki, unapungua kila mwaka. Hii naisema, siyo maneno yangu, ni maneno ya utafiti ambao umefanyika. Utafiti wa mapato na matumizi ya kaya binafsi uliofanyika mwaka 2018 na Mheshimiwa Waziri Mkuu akauzindua utafiti huu, unaonesha kwamba umasikini wa kipato umepungua kutoka asilimia 28.2 toka mwaka 2012 na sasa umefika asilimia 26.8 mwaka 2018. Hivyo siyo sahihi kuendelea kuimba wimbo wa Taifa letu kwamba watu wanazidi kuwa masikini. Siyo sahihi hata kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti huu pia unaonesha umasikini wa chakula kwa Watanzania katika kila kaya, mwaka 2012 ulikuwa asilimia 9.7; mwaka 2018 umasikini wa chakula kwa kaya ya kila Mtanzania ni asilimia 4.4. Kwa hiyo, tunaomba Watanzania wafahamu kwamba jitihada za Serikali yao na wao Watanzanzia wamejitolea kuelewa jitihada hizi za Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali yake wanafanya kazi kwa jitihada zote. Umasikini wa kipato na umasikini wa chakula umepungua kutokana na tafiti zilizofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili kwamba tuwekeze kwenye viwanda ambavyo vinatumia rasilimali watu zaidi kuliko kutumia capital intensive. Naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba katika viwanda ambavyo vimeanzishwa na vinaendelea kujengwa kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri wa uwekezaji asubuhi, ni viwanda vinavyotumia zaidi rasilimali watu. Viwanda hivi ni vile ambavyo vipo katika maeneo ya nguo. Tunafahamu hatujafanya vizuri zaidi, lakini jitihada zinaendelea kufanyika. Viwanda vya kutengeneza tiles havitumii mashine, vinatumia rasilimali watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vingine ni vya kuchakata mazao yetu, havitumii capital, vinatumia zaidi rasilimali watu. Nawaomba Watanzania wanaomaliza Vyuo Vikuu waweze kwenda kufanya kazi kwa tija kwenye viwanda hivyo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali, katika jimbo langu la Bunda kuna maboma ya maabara na hasa katika Shule ya Sekondari Salama. Mheshimiwa Waziri hatudhuliani ni ndugu yangu, katika ile shule kumekuwepo na maboma mawili ambayo kuna mabati na mbao zinaenda kuonza ni muda mrefu, wananchi hali yao ni mbaya wamekuwa na michango mingi kwenye maeneo mbalimbali. Nakuomba Waziri hili ni ombi rasmi nakuomba Waziri unisaidie kunipelekea milioni 30 tu kwenye shule ya sekondari salama ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue ombi la Mbunge Boniphace kwa sababu nikifahamu eneo lake lile kwa kweli kuna changamoto nyingi mbalimbali na nikiri wazi kwamba eneo hilo lazima tulipe kipaumbele kwa sababu kuna fedha tu kidogo zinahitajika tutaangalia mfuko ukoje halafu tutashirikiana mimi na wewe kuangalia jinsi gani tutafanya kuhakikisha hiyo miundombinu ambayo wananchi wamejitolea isiweze kuharibika.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza niishukuru Wizara ya Maji, Waziri wake, Naibu na Katibu Mkuu wake kufanya juhudi hizo za kupeleka wataalam kwenye Jimbo hilo la Bunda ambalo lina uhaba mkubwa sana wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa maji yamepatikana katika maeneo 10 ambayo ameshayataja hapa awali na kwa kuwa hizi ahadi zimeanza 2016/2017 mpaka leo 2019. Swali langu la kwanza katika eneo hilo ni kwamba Wizara inazo fedha tayari za kutengeneza mradi wa kuchimba Malambo matano kwa mwaka huu au ni ahadi zile zile za mwaka uliopita? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mheshimiwa Rais tarehe 6 Septemba, 2018 alifika kwenye Jimbo langu kwenye Kata ya Nyamuswa na akiwa Nyamuswa alipata kero kubwa sana ya maji kutoka kwa akinamama wa Nyamuswa ambao wanakabiliwa na kero kubwa sana ya maji. Aliagiza Waziri wa Maji tarehe 6 Septemba, 2018 kwamba baada ya wiki moja Waziri afike pale ahakikishe kwamba anakaa na wanakijiji wa pale akinamama na wadau wa maji wote kwenye Kata ya Nyamuswa kuhakikisha kwamba maji yanapatikana. Sasa ni miezi tisa, Waziri hajaenda pale lakini sio mbaya.

Je, Naibu Waziri ambaye uko sasa ambaye ni Waziri wewe sasa hivi, uko tayari kwenda Nyamuswa kushughulika na lile agizo la Rais? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, amekuwa mfuatiliaji mkubwa sana hususan katika suala la maji katika Jimbo lake la Bunda lakini nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge. Sisi ni Wizara ya Maji, sio Wizara ya Ukame na hii ni Serikali ya Awamu ya Tano ikiahidi inatekeleza na ikishindwa kutekeleza basi kuna kuwa na sababu mahsusi kabisa katika utekelezaji wake.

Nataka nimhakikishie na ndiyo maana tumetuma wataalam wetu ili kuhakikisha kwamba zile tathmini zilizofanyika ili tuanze utekelezaji ili wananchi wako waweze kupata huduma ya maji. Tunakuomba Mheshimiwa Mbunge utupe ushirikiano wa dhati ili tuhakikishe kwamba wananchi wako yale mabwawa matano tunakwenda kuchimba, ili wananchi waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu kufanya ziara katika jimbo lake kwa Mheshimiwa Mbunge, niko tayari kabla ya Bunge, ili kuhakikisha tunakwenda kutatua tatizo hilo ambalo limeahidiwa. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza naipongeza Serikali kwa majibu mazuri waliyoyatoa, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa utafiti na maeneo mengi yanaonyesha kwamba bodaboda wengu katika nchi na hasa kwa Mkoa wa Mara wanafanya kazi ile bila kupata mafunzo rasmi ya kazi yao. Sasa ni lini Serikali itatoa mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu kwa vijana wote wanaoendesha bodabora katika Mkoa wa Mara?

Swali la pili, kwa jimbo langu la Bunda na hasa Wilaya ya Bunda kumekuwepo na usumbufu mkubwa wa bodaboda wakati wa siku za minada, hasa Mnada wa Mgeta, Bitalaguru na mnada wa Bulamba. Sasa je, Waziri uko tayari kuja Bunda na hasa Jimbo la Bunda kukutana na viongozi wa bodaboda na watalaam wako wa traffic katika jimbo la Bunda ilikuona namna gani ya kutatua kero hiyo hasa siku za mnada inakuwa kama inafanya operation?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeza sana Mheshimiwa Mwita Getere, nakumbuka niliwahi kufanya ziara katika jimbo lake tulishirikiana kwa karibu sana kuhakikisha kwamba changamoto ambazo zinawakabili wananchi wake zinazohusu vyombo vyetu vinavyohusu Mambo ya Ndani ya Nchi tunavikabili.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba hata katika hili suala ambalo amelizungumza la usumbufu wa wananchi wake kwenye minada na amenitaka niende basi namhakikishia kwamba nitafanya hivyo kama ambavyo nilifanya wakati ule.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusiana na mafunzo kwa Mkoa wa Mara tumekuwa na utaratibu mzuri kupitia Jeshi la Usalama barabarani kwa kutoa mafunzo watumiaji wa vyombo vya usafiri barabarani. Hata hivyo nichukue nafasi hii kumhakikishi kwamba kwa kuwa nitakwenda katika jimbo lake basi tunaweza kushauriana kuwa mpango mahususi wa jimbo lake kuhusiana na utararibu wa kutoa elimu ili kuepusha usumbufu kwa wananchi wake au hususani vijana wanaendesha bodaboda waweze kutii sheria na kuepusha usumbufu na hatimaye kupunguza ajali zinaendelea kupoteza maisha ya wananchi.
MHE. BONIFACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tunamshukuru Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kutupa barabara ya Makutano - Sanzate na kuna kipande cha Sanzate cha kwenda Nata - Mugumu na barabara ya Nyamswa - Bunda, Bunda - Buramba, Buramba - Kisorya.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Makutano - Sanzate kama ni mkandarasi amepewa nafasi ya kumaliza barabara hi ni zaidi ya mara saba na tarehe 06.09.2018 Mheshimiwa Rais ameenda pale na akaagiza barabara hii imalizike haraka iwezekanavyo.

Sasa ni nini kifanyike sasa ili barabara hii ikamilike kwa sababu kama mkandarasi ambae tunamuita wazawa amepewa fedha, ana vifaa, ana wataalam lakini barabara haiishi. Nini kifanyike barabara hii ikamilike?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kuna barabara ya Mgeta - Sirorisimba ambayo TANROADS waliitengeneza ikabaki kilometa tisa. Nilikuwa namuomba Waziri sasa atamke kwamba hiki kipande cha kilometa tisa kitaisha lini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze tu Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa akifuatilia sana hii barabara lakini pia hiyo barabara aliyoitaja ya kutoka Mgeta - Sirorisimba. Ninampongeza sana na niwashukuru tu Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Mara kwa sababu siku ya Jumatano nilijibu swali kama hili hili, swali namba 377 la Mheshimiwa Agness Marwa kuonesha namna wanavyoshirikiana, lakini kuonyesha barabara hii ni kipaumbele kwenye Mkoa wa Mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini kifanyike; kweli kumekuwepo na changamoto muda mrefu wa ukamilishaji wa barabara hii lakini labda nipende tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna sehemu ya kilometa 18 ilikuwa ina shida mpaka tulilazimika kubadilisha design kwa maana ile barabara ya kutoka Makutano kuja Butiama kilometa 18. Ni sehemu ambayo ilikuwa ni korofi, ni sehemu ya mlima ilikuwa na mawe mengi, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi sasa ninavyozungumza changamoto ile mkandarasi ameiondoa kwa maana yale mawe ameshayatoa na kilometa 13 sasa ameshaweka tabaka la sub-base kwa maana ya kwamba cement na mchanga wameweka kilometa 13 na kilometa sita wameshaweka base.

Nikuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi ni kwamba sasa kufikia Januari kama makubaliano ambayo watayakamilisha kesho, kesho kutakuwa na kikao kati ya mkandarasi na uongozi wa TANROADS Makao Makuu kwa maana ya kuijadili barabara hii muhimu. Vuta subira Mhehsimiwa Mbunge nitakupa feedback kwamba hayo makubaliano yatakuwa ya mwisho kuhakikisha kwamba tunakubaliana na barabara hii inakwenda kukamilika, kwa hiyo, usiwe na wasiwasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu barabara ya Mgeta - Sirorisimba; zipo kilometa 22 katika barabara hii. Kimsingi barabara hii inasimamiwa na TARURA, lakini kulikuwa kuna ombi maalum la Mheshimiwa Mbunge ndiyo maana nilianza kwa kumpongeza ili sasa upande wa TANROADS kuweza kusaidia barabara hii muhimu na barabara hii kilometa 22 ulifanyika ujenzi wa kuweka kokoto kilometa zote 22; lakini kuna maeneo ambayo barabara ilipanuliwa na kuweka makalavati makubwa kama sita hivi kilometa zile 13 na ikabakia kilometa tisa ambazo Mheshimiwa Mbunge unaulizia hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na niseme tu kwamba tumekubaliana na nielekeze pia zaidi watu wa TANROADS Mkoa wa Mara hizi kilometa tisa maeneo ambayo yalikuwa yamebakia kama ni korofi waweze kumalizia na natumaini pia upande wa TARURA kuna fedha wametenga kwa ajili ya kufanya maboresho. Na niwahakikishie wananchi wa Mgeta na Sirorisimba kwamba barabara hii tunaijali na mimi mwenyewe binafsi nimefika maeneo haya na nimeongea pia na Wananchi wa Sirorisimba na Mgeta wameridhika kwa kiwango kikubwa kazi iliyofanyika kwa hiyo Mheshimiwa Getere nafahamu na unafahamu kwmaba tunafanyakazi nzuri katika maeneo yako.
MHE. BONIFACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la kwanza kwenye Bunge lako hili la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Spika, suala la madawati limekuwa ni suala sugu sana katika nchi yetu. Swali langu la kwanza, nataka kujua Serikali ina mpango gani sasa wa kuwa na mfuko maalum au mfuko wa kudumu ambao utafanya hili tatizo la madawati liweze kupungua katika nchi yetu na hasa katika Jimbo langu la Bunda, upungufu wa madawati kwenye shule za msingi na sekondari ni mkubwa sana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, sasa hivi nchi yetu kuna wanafunzi wanaenda shuleni hasa sekondari. Kuna mkanganyiko wa kusema twende na madawati, wengine wananunua wazazi, wengine wanasema Serikali inaleta.

Mheshimiwa Spika, nini tamko la Serikali kwenye suala hili la madawati katika shule za sekondari? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE: DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nimjibu Mheshimiwa Boniface Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, maswali yake mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza, ametoa kama pendekezo la Serikali kuanzisha mfuko maalum kwa ajili ya kutatua tatizo la madawati. Jambo hili nafikiri ni jambo jema na sisi kama Serikali tunalipokea. Hata hivyo, pamoja na kupokea wazo ambalo amelileta la kuwa na mfuko maalum, lakini bado naweza kueleza kwamba hili suala la upungufu wa madawati mashuleni Serikali imeendelea kukabiliana nalo, lakini na sisi kama Wabunge tuna wajibu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, moja, kwanza sisi Wabunge ni Madiwani katika Halmashauri zetu. Pia katika halmashauri tunapswa kuwa na mipango ya kutumia fedha za ndani kuhakikisha kila mwaka tunatenga fedha kwa ajili ya kutatua tatizo la madawati.

Mheshimiwa Spika, vilevile sisi ni Wenyeviti wa Mifuko ya Jimbo. Kwa hiyo, kama kuna changamoto katika halmashuri yako sehemu ya fedha za Mfuko wa Jimbio unaweza kuzitumia katika kutatua tatizo la madawati. Aidha, unaweza kutafuta wadau mbalimbali ambao wanaweza kusaidia kuhakikisha kwamba tunaondoa changamoto hiyo.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kuhusiana hoja kwamba watu wengi wamekuwa wakilazimishwa ili mwanafunzi aingie darasani lazima mpaka ulipe mchango wa dawati ama utoe dawati. Msimamo wa Serikali ambao aliutoa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ni kwamba wanafunzi wote wanapaswa kujiunga bila kuwa na masharti, kama hilo linaloletwa la kusema kwamba lazima mtu atoe dawati ndiyo asajiliwe shuleni.

Kwa hiyo, msimamo wa Serikali bado uko palepale na tutaendelea kusimamia huo msimamo wa Serikali kama ambavyo Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ameagiza. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika swali langu la msingi nimesema kwa kuwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi imefanya kazi nzuri ya kutoa elimu bure katika shule za msingi mpaka sekondari; na kwa kuwa Waraka wa Serikali Namba 5 wa 2015 unasema, elimu bure ni kutoka shule ya msingi mpaka sekondari; na kwa kuwa kidato cha tano na kidato cha sita ni sekondari, ni kitu gani kinazuia Serikali kutoa elimu bure kwa kidato cha tano na cha sita kwa sababu ni sekondari hiyohiyo ambayo inazungumzwa?

Mheshimiwa Spika, umesikia Wabunge wengi wanasema hapa, Mheshimiwa Oliver, Mheshimiwa Sanga na wengine kwamba imetajwa katika Waraka kwamba elimu bure ni shule ya msingi mpaka sekondari, kidato cha tano na cha sita ni sekondari. Sasa ni lini Serikali itatoa elimu bure kwa kidato cha tano na cha sita?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tumezungumza humu mara nyingi sana na hili swali naliuliza kama mara ya tano sasa, Shule ya Sekondari za Unyali, Mkomalilo, Mihingo, Esparanto, Makongoro, Wamamta, Salama, hazina walimu wa sayansi. Watu wanachanga, tumejenga majengo mazuri watoto wanasoma lakini hawana walimu. Lini Serikali itapeleka walimu kwenye shule hizi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Waraka Namba 5 wa mwaka 2015 wa Elimu Msingi, unaelekeza kwamba itakuwa elimu bure kuanzia elimu ya awali mpaka kidato cha nne. Mheshimiwa Mbunge anauliza kwa nini kidato cha tano na cha sita hakipo katika mpango huo. Ni kweli, kidato cha tano na cha sita hakipo kwenye mpango huu lakini naomba nilieleze Bunge lako tukufu kuwa tunaendelea kuboresha bajeti yetu ya Serikali, mpango huu unaweza kufikiwa iwapo tu bajeti ya Serikali itakuwa imekaa sawasawa.

Mheshimiwa Spika, kama mnavyofahamu, baada ya kupata fursa hii ya kutoa elimu bure usajili wetu wa wanafunzi, tuchukulie mfano wa darasa la kwanza, umeweza kuongezeka kutoka wanafunzi 1,300,000 mwaka 2014 mpaka wanafunzi 2,070,000 mwaka 2016/2017. Utaona kuna ongezeko hilo kubwa kutokana na Sera hii ya Elimu Bure. Kwa hiyo, upatikanaji wa fedha utatupeleka kuhakikisha kwamba kidato cha tano na cha sita tunawaingiza katika mpango huu.

Mheshimiwa Spika, halikadhalika napenda kueleza kwa zile kaya ambazo ni maskini tuna mpango wetu wa TASAF ambapo kwa mwanafunzi wa shule ya msingi anapata shilingi 12,000/= kwa mwezi na wale wa sekondari wanapata shilingi 16,000/= kwa mwezi. Hawa wanaweza wakasaidiwa katika mpango huu ili kuhakikisha kwamba tunaweza kufikia yale malengo ya kulipi hiyo ada ndogo ambayo inalipwa katika kidato cha tano na cha sita.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili, shule alizozitaja na hasa kuhusu wale walimu wa sayansi, Mheshimiwa Waziri Mkuu hapa ametoka kujibu swali kama hilo katika kipindi kifupi kilichopita, Serikali tayari imeshaanza mpango wa kuajiri walimu. Katika mwaka 2020 tumeajiri zaidi ya walimu 8,000 wameshapelekwa shuleni. Sasa hivi Serikali iko kwenye mchakato wa kuajiri tena walimu 5,000 ambao katika kipindi kifupi kijacho tunaamini shule hizi alizozitaja zinaweza zikapata hao walimu wa sayansi.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushuru Mheshimwa Spika, kwa kunipa nafasi ya kuuliza. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa chande kwa kuteuliwa kupata nafasi hiyo, tunakuombea kwa Mungu akusaidie ili uweze kuona mbele zaidi, kwake nina swali moja tu. Kwa kuwa humu ndani ameandika sheria nyingi za mazingira, sasa swali ni lini atafika kwenye Jimbo la Bunda kwenye Vijiji vya Nyabuzume, Jabulundu na maeneo yaliyoharibiwa na barabara inayojengwa ya lami kutoka Butiama -Nyamswa na Sanzati ili kuangalia athari za mazingira katika maeneo hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, siku za karibuni mara tu baada ya Bunge kumalizika tutafuatana mguu kwa mguu mimi na yeye twende kuangalia hali hiyo na insha Allah tutekeleza. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza; kwa kuwa eneo lote lile la mlima lilikuwa la kijiji na kwa kuwa sheria zetu za ardhi haziruhusu mtu kwenda kuvamia kijiji au Kamati ya Ulinzi kwenda kutwaa eneo la kijiji na kuligawia taasisi nyingine, ile ni mali ya wanakijiji.

Sasa ni lini taasisi hiyo iliyotwaa eneo la wanakijiji watalipa fidia ya kaya 10 ambazo zilikuwa zinafanya kazi pale? Hilo swali la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa migogoro ya ardhi Mkoa wa Mara imekuwa mingi sana na hata juzi tumesikia Rorya pale kuna mtu amekufa kwa migogoro ya ardhi. Ni lini sasa Serikali itaenda kupima hasa vijiji 30 vya Tarafa ya Chamriho, Jimbo la Bunda kuwapa Hati ya Kimila?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Getere kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza Sheria ya National Environmental Management Act No. 20 ya 2004 hairuhusu maeneo yale ambayo ni hatarishi kama milima na maeneo ya kingo za mito kuweza kumilikiwa na wananchi, yanakuwa ni protected chini ya usimamizi wa Waziri wa Ardhi. Kwa hiyo, eneo la mlima analolizungumzia si halali kwa watu kumilikishwa pale na litabaki under protection kama ambavyo Kamati ya Usalama ya Wilaya imekwishaelekeza kuwapa watu wa Magereza kuliangalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusiana na vijiji 30 kuhusu suala zima la kuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi; kama nilivyojibu juzi, ni suala tu la mamlaka yenyewe ya upangaji, pale watakapokuwa tayari sisi kama Wizara kupitia Tume ya Mpango wa Matumizi ya Ardhi tutakuwa tayari kushirikiana nao kwa sababu kadri wanavyopima na kuweka mpango wa matumizi katika vijiji vyao, ndivyo jinsi ambavyo wanapunguza migogoro ya ardhi kwa watumiaji ardhi katika maeneo. Kwa hiyo, sisi tupo tayari wakati wowote pale ambapo Halmashauri itakuwa tayari kufanya kazi hiyo, waangalie kama bajeti wanayo, tutakwenda kuwasaidia, ahsante.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nilipata fursa ndani ya kipindi cha mwezi mmoja uliopita nilienda kutembelea eneo hilo na bahati nzuri tulikuwa na Mbunge husika na zile kaya tuliweza kuzibaini pale katika eneo lile. Tulichokifanya na Kamati ya Ulinzi na Usalama chini ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya tukasema kwamba wale ambao kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira maana yake hakuna compensation isipokuwa nini utaratibu wa busara ufanyike.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, jambo hilo tumeliacha chini ya Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, DC wetu wa Tarime linafanyiwa kazi lakini utaratibu wa kulitangaza eneo lile kuwa eneo lindwa, utaratibu huo kwa mujibu wa Kanuni zetu tunaenda kubadilisha Kanuni hivi sasa si muda mrefu tutatangaza baadhi ya maeneo likiwemo eneo la Mlima Nkongore, ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza swali la kwanza nilitaka kujua tu kwa kuwa Mkoa wa Mara ardhi yake ina hali ya hewa nzuri ya zao la Alizeti, na hasa katika tarafa ya Chamriyo Wilaya ya Bunda yenye vijiji 30 na kata saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini sasa Serikali kwakuwa inataka kupunguza uhaba wa mafuta ya kula hapa Tanzania ni lini itapiga kambi pale kwenye Tarafa ya Chamriyo yenye vijiji 30 na kata saba yenye hali ya hewa nzuri ya kulima Alizeti ili kuwapa mbegu bora za kulima Alizeti na kupunguza uhaba wa mafuta hapa Tanzania?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa kuwa katika swali lako la msingi umezungumza kwamba Maafisa ugani watapewa pikipiki na vitendea kazi vingine Je, kwa Mkoa wa Mara ambao upo tayari kulima Alizeti ni lini vitendea kazi hivi navyo vitafika kwa maafisa ugani wa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza maeneo yote ambayo yana-potential ya kuzalisha Alizeti au mazao yote ambayo yatatusaidia kupunguza tatizo la mafuta tutayapa kipaumbele kama Serikali, na nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge tunaweza kukaa mimi na yeye na tukajadiliana namna gani tunaweza kuanzisha mfumo wa Block farm katika Wilaya ya Bunda, na kwasababu wenyewe wanazalisha pamba, na pamba ni moja ya zao ambalo tunalipa kipaumbele. Kuhusu vitendea kazi ni kwamba kwanza bahati nzuri Mheshimiwa Mbunge anatoka kwenye ukanda wa Pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kupitia bodi ya pamba sasa hivi tumeanza program ya kuwapatia Maafisa Ugani Elimu na vitendea kazi kwenye ukanda wote unaozalisha pamba na Bunda ni moja wa Wilaya na hivi sasa tunavyoongea bodi ya pamba imeanza kukutana na Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Wilaya zinazozalisha pamba ili maafisa Ugani waingizwe kwenye program ya kupatiwa vitendea kazi lakini vile vile kupatiwa vifaa soil analysis kit ambazo watatumia kuwa wanapima afya ya udongo katika maeneo hayo. Kwa hiyo, Wilaya ya Bunda na Mkoa wa Mara ni moja ya Mkoa ambayo kwetu ni potential na tutaipa kipaumbele.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali, barabara ya kutoka Makutano, Butiama Nyamswa na Sanzati ni barabara imejengwa kwa muda mrefu sana mkataba wake ulikuwa miaka miwili sasa ni miaka minane toka imeanza kujengwa kama ni bajeti ilikuwa na bajeti ya shilingi bilioni 46 sasa inaenda mpaka Bilioni 50 ni lini sasa hiyo barabara itakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI – (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba barabara hii imechukua muda mrefu ni miongoni mwa miradi ya barabara ambayo ilikuwa na mkwamo na Mheshimiwa Mbunge anajua kwamba changamoto zimetatuliwa barabara inaendelea kujengwa na kazi itakwisha matarajio mwaka huu kabla haujakwisha hadi mwaka ujao itakuwa imeshakamilika barabara hii, na tumepanga baada ya Bunge kukamilika tutaenda kutembelea barabara ile ili kuona hali halisi katika eneo la ujenzi. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali.

Mheshimiwa Spika, haya mambo ya wanyamapori mimi naona kwamba sasa tunapokwenda tutabakiza nchi ya wanyamapori. (KIcheko)

Sasa mimi najiuliza hivi ni tembo wangapi wanatosha kuishi katika mapori ya Tanzania ambayo watalii watakuja kuona, kwa sababu kama tembo hawa hawana uzazi wa mpango maana yake sasa tuwaruhusu waishi kwa wananchi, ni tembo wangapi wanatosha ili watalii waone kwamba hawa tembo wametosha tunakwenda kuwaona. Maana yake tunapoamini tembo wakiwa wachache ndio watalii watawatafuta, sasa wakiwa wengi … kwenye utalii gani?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba nimpe tathmini ya idadi ya tembo mpaka sasa; mwaka 2009 kulikuwa na idadi ya tembo 134,000 lakini kabla ya hapo walikuwa wanafika tembo 300 na kadhalika, lakini walishuka mpaka kufikia 134,000. Toka mwaka 2009 mpaka 2014 ambapo kulikuwa na poaching kubwa, tembo walishuka mpaka wakafika 43,000. Kutoka mwaka 2014 mpaka 2020 wanakadiriwa sasa
wameongezeka kufika 60,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utaangalia hata ile idadi ya mwaka 2009 bado hatujaifikia; kinachotokea hapa ni kwamba tembo anahamasika hasa kipindi cha mavuno, anaweka kambi kwenye maeneo ambayo ni shoroba zao na anapoweka ile kambi basi wanahamasika kula mazao ambayo pengine huyu tembo toka azaliwe hajawahi kukutana na hindi, muhogo anahamasika ndiyo maana sasa changamoto sasa hivi imekuwa ni kubwa kwa sababu ni kipindi hiki hasa cha mavuno, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nakuomba katika swali hili utupe msaada, maana sasa tunahitaji msaada wako.

Mheshimiwa Spika, mwezi wa pili mwaka huu 2021 tulikuwa na Waziri wa Ujenzi pale Butiama na Mkuu wa Wilaya ya Butiama alileta meseji ya Mama Maria kwamba anazunguka mno kutoka Musoma kuja kule mpaka apitie Kyabakari eneo lake limeshindwa kukamilika. Hii barabara Mkandarasi alipewa 2013 amalize 2015, miaka miwili hakumaliza;2015 -2017 hakumaliza; 2017-2019 hakumaliza; na 2019-2021 hajamaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi tulikuwa na Waziri wa Ujenzi nikamwambia huyu hatamaliza. Sasa hii miradi inayopita Butiama pale kuna shida gani? Katika mradi ambao unatia aibu katika Mkoa wa Mara ni mradi huu wa barabara. Tunaomba msaada wako, yule Mkandarasi hatamaliza ule mradi, hilo ni suala la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mkandarasi yule ameshindwa hata kwenda site mpaka sasa hivi. Toka tulipoongea na Waziri mwezi wa Pili, aliondoka mpaka leo. Barabara ya diversion ya kupita kwenye ile barabara haipitiki: Je, Waziri au Serikali ipo tayari kuwaambia TANROADS wa Mkoa wa Mara waende wakatengeneze diversion ya ile barabara? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni mradi wa aibu, naomba msaada wako. (Makofi)
WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara hii ilipewa Mkandarasi huyu kwa muda mrefu uliopita na kama ilivyojibiwa katika jibu la msingi barabara hii ilipewa Wakandarasi hawa wazawa kama barabara ya kuwajengea uwezo. Tumekuwa tukiendelea kuwajengea uwezo hao lakini ilitokea changamoto mbalimbali ambazo tunaendelea kukabiliana nazo.

Mheshimiwa Spika, changamoto ambazo zilijitokeza ambazo zilikuwa ni ngumu kidogo kwa Wahandisi wapya wazawa ni baada ya kukutana na miamba ambayo ni dhaifu ambapo ilibidi wahangaike kutafuta miamba ambayo ni migumu kidogo. Kwa hiyo, tumekuwa tukishirikiana nao katika kuwajengea huo uwezo wa kutafuta miamba migumu ili kuweza kukabiliana na barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, nilichukua fursa hiyo ya kwenda mwenyewe kufanya ule ukaguzi na Mheshimiwa Mbunge tulikuwa naye na tukaahidiana kwamba tutaweza kulishughulikia jambo hilo kwa haraka ili usiwe ni mradi wa aibu.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa tunaendelea vizuri na tayari tumeshamwambia yule Mkandarasi na ameshatekeleza kupata kokoto mbadala kutoka sehemu ambayo inapatikana na tunaendelea kuwahimiza ili waweze kumaliza katika hii miezi minne ambayo tumewaongezea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, japokuwa ni kweli kwamba mradi huu umechelewa, tayari tumeshachukua hatua muhimu za kuhakikisha kwamba mradi huu utakamlika kwa wakati na usiwe mradi wa aibu na Wakandarasi wazawa tuendelee kuwajengea uwezo ili waendelee kuaminika katika miradi kama hii. Naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na majibu ya Serikali nimeyaona lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria ulioanza mwaka 2005 ukamalizika mwaka 2018, ambao ulikuwa unatoa maji Ziwa Victoria kuleta Bunda Mjini, na kwa kuwa mradi huo ulikuwa umejumuisha vijiji 30 ambavyo leo tunaviuliza hapa, na kwa kuwa bajeti ya mwaka 2020/2022 imeonyesha kwamba Jimbo la Bunda Vijijini litapewa maji ya Ziwa Victoria kutokea Bunda Mjini. Swali la msingi hapa ni lini sasa Waziri wa Maji ataenda Jimbo la Bunda Vijijini kutangaza mradi huu ambao ameugusia kwenye bajeti ya 2021/2022? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali imetumia milioni 40 kufanya utafiti wa vijiji sita ambavyo vina uhaba wa maji kwenye maeneo hayo na maeneo hayo ni Mihingo, Tingirima, Rakana, Jaburundu, Salama A, Kambubu. Serikali imetumia milioni 40 kutengeneza tathmini ya mkakati wa kuchimba na makinga maji kama malambo ya maji hayo. Ni lini sasa itaenda kukamilisha mradi huo ambao uko hapo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda sana kumpongeza Mheshimiwa Getere kwa ufuatiliaji wa karibu sana na kwa namna ambavyo tumeendelea kushirikiana naye. Nipende kumuambia tu Mheshimiwa Getere kwamba, suala hili la Bunda kuweza kutumia maji ya Ziwa Victoria ni suala ambalo ni la kimkakati Kiwizara na tunafahamu maji yameshafika pale Bunda Mjini na kwa eneo lake la Bunda Vijijini, Serikali ipo katika mkakati wa kuona kwamba mipango yetu ya muda mrefu inakwenda kufanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na baada ya Bunge hili Wizara itatuma wataalamu pale kwenda kuangalia uwezekano wa kutumia yale maji yaliyofika Bunda Mjini na ikishindikana, basi watafanya review mpya kabisa kuona kwamba sasa maji kutoka Ziwa Victoria yanafika Bunda Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na swali lake la pili la kuhusiana na malambo sita ni kweli, Serikali tulipeleka milioni 40 na malambo yale tutakwenda kuyajenga awamu kwa awamu. Tayari lambo la kwanza lipo kwenye utekelezaji asilimia 40 lakini shughuli za ukamilishaji wa lambo hili, utaendelea baada ya mgao ujao wizara kupeleka fedha na kuhakikisha malambo yote sita kila tunavyopata fedha tutapeleka ili yaweze kukamilika. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Hili suala la wastaafu kwa kweli ni kero kubwa katika nchi yetu. Nashukuru majibu ya Serikali, lakini niseme tu Serikali inatakiwa kujitahidi kwenye jambo hili, kwa sababu wastaafu waliomaliza ku-document document zao ambao wapo kwenye maeneo, wanaolia, wanaokwenda kwenye maofisi, wana miezi sita, miaka tano, miaka minne, ni wengi kuliko ilivyo kawaida.

Kwa hiyo, Serikali itafute mfuko thabiti wa kuzingatia mambo haya ili watu waweze kupata fedha zao. Watu wanakufa wanadai fedha, kwa nini mtu ameitumikia nchi, halafu anakufa anadai fedha.

Mheshimiwa Spika, naiomba tu Serikali itengeneze jambo hili liwe nzuri zaidi.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA NA WATU WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri na Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma. Naomba niliambie Bunge lako Tukufu, Serikali ya Awamu ya Sita na hasa Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma baada ya kuingia na kugundua kwamba wakati mwingine ucheleweshaji wa mafao hayo ya wastaafu yanatokana na haya malimbikizo ya michango. Michango mingi ambayo inatakiwa ipelekwe na waajiri, imekuwa ikicheleweshwa kupelekwa kwa mazingira ya aina moja ama nyingine. Serikali imekuja na suluhu hiyo ya kutengeneza mfumo ambao utawasaidia wafanyakazi wote kutambua ni lini wanastaafu na haki zao zikoje?

Mheshimiwa Spika, ili kurahisisha sasa na upande wa pili wa mifuko, tumewaagiza na wameshatekeleza. Kwa mfano, Mfuko wa PSSSF wameshatengeneza mfumo ambao unaitwa PSSSF Kiganjani. Mfumo huo sasa umeshasambazwa na unaendelea kusambazwa kwa wanachama wote. Wanachama ambao wanakaribia kustaafu, wamekuwa sasa wakiwezeshwa kuzitambua haki zao kupitia kwenye mfumo na kuanza kuwasiliana na ofisi zote kabla ya muda kustaafu ili kupunguza hiyo kadhia ambayo imekuwa ikiendelea.

Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo tumewahagiza Mfuko wa PSSSF na mifuko mingine, kabla ya muda wa kustaafu, wastaafu wote watarajiwa tumeanzisha sasa vikao maalumu mfuko kukutana na wastaafu watarajiwa kuwatambua na kuandaa mafao yao mapema na hivyo kadiri tunavyokwenda kadhia hii itakuja kuondoka na tunapenda wastaafu waweze kupata mafao yao kwa muda unaotakiwa. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuku kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ningependa kujua kituo cha polisi Mgeta ambacho niliahidiwa kujengwa na niliambiwa nilete tathmini ya ujenzi wa kituo hicho ambacho wananchi wamejenga, tumefikia kwenye boma. Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani na Naibu mwenye waliniahidi kwamba ikifika mwezi Agosti, 2021 kitakuwa kimeshamalizika kujengwa. Ni lini sasa watakwenda kumaliza hiyo ahadi yao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwita Getere nalo nalijibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tulifika wakati tukaona kwamba tunaweza tukapata fedha haraka kwa ajili ya ujenzi wa kituo kile, lakini mambo yaliingiliana kwa sababu tuna nyumba za maaskari, tuna vituo vya polisi, tuna mambo mengi ambayo polisi tunahitaji tuimarishe ili wananchi waweze kupata huduma hizo. Kubwa nimwambie tu kwamba katika mwaka wa fedha ujao tutajitahidi kituo kile tukiangalie, tutakipa kipaumbele ili wananchi waweze kupata huduma za ulinzi na usalama. Nakushukuru.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nilipenda kujua tu kwamba Waziri anayezungumza hapa ndiyo mwenye mamlaka ya kugawa mipaka ilivyo kati ya wananchi na wanyamapori. Sasa nimuombe Mheshimiwa Lukuvi mpaka wa vijiji kama 11 hivi vya Jimbo la Bunda ukianzia mipaka ile ya Honyali, Maliwanda ukienda Mgeta mpaka Tingirima mpaka wao ni Mto Rubana ndiyo mto asili unaotumiwa na wananchi wa maeneo yale lakini mpaka uko katikati ya Mto Rubana. Ni lini Waziri ataenda pale kutenganisha mita 500 za wanyamapori na mita 500 za wananchi?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Getere kwanza nitamuona hapa hapa anipe ufafanuzi vizuri zaidi lakini pia ninao uwezo wa kwenda Mkoa wa Mara kwenda kuzungumza nae na viongozi wengine ili tujue hilo kwa sababu hata vijiji huwa vinaanzishwa kwa mfumo ule ule unaofanywa na Wilaya na Mikoa.

Mapendekezo ya kuanzisha vijiji huwa yanaanzia Wilayani yanakuja mkoani mwishoni Ofisi ya Rais, TAMISEMI ndiyo inaidhinisha ambayo iko chini ya Ofisi ya Rais na kutoa GN maandishi yanayoainisha kila Kijiji na mipaka yake iko namna gani. Jukumu langu mimi siyo kuanzisha mipaka ya vijiji vipya Wizara ya Ardhi hatuanzishi mipaka, tunasuluhisha lakini kwa kutafsiri ardhini GN za mipaka zilizoainishwa na mamlaka inayohusika.

Kwa sababu hiyo, nitakwenda huko kwenda kuwasaidia wananchi wa vijiji hivyo kuainisha mipaka iliyopendekezwa au iliyoamuliwa kuaanzisha vijiji hivyo kwa mujibu wa mapendekezo ya mamlaka. Lakini pia hiyo migogoro kati ya buffer zone na ardhi za vijiji nitapenda kumsikia lakini tutakwenda huko hivi karibuni tulikwenda Serengeti nako kulikuwa na migogoro ya buffer zone vijiji vilivyoanzishwa hifadhi ya Serikali ilichukua mita 500 za ardhi ya vijiji ikafanya buffer zone.

Rais wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameagiza ili kuondoa taharuki, ardhi ile ambayo Serengeti walichukua kuanzia Mkoa wa Mara kule Tarime mpaka Serengeti mita 500 kwenye ardhi za vijiji zirudishwe kwenye vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumetekeleza maelekezo hayo mita 500, 500 zilizokuwa kwenye buffer zone ya Hifadhi ya Serengeti zimerudishwa kwenye vijiji na hivyo Serengeti sasa kama wanahitaji buffer zone watarudi ndani ya hifadhi yao. Lakini zile za vijiji zimerudishwa tayari, kwa hiyo hili nalo tutakwenda kujifunza nature ya mgogoro huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Rais wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameagiza, ili kuondoa taharuki, ardhi ile ambayo Serengeti walichukua kuanzia Mkoa wa Mara kule Tarime mpaka Serengeti, mita 500, kwenye ardhi za vijiji zirudishwe kwenye vijiji.

Mheshimiwa Spika, tumetekeleza maelekezo hayo, mita mia tano mia tano zilizokuwa kwenye buffer zone ya Hifadhi ya Serengeti zimerudishwa kwenye vijiji na hivyo, Serengeti sasa kama wanahitaji buffer zone watarudi ndani ya hifadhi yao, lakini zile za vijiji zimerudishwa tayari. Kwa hiyo, hili nalo tutakwenda kujifunza nature ya mgogoro huu.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inafanya kazi nzuri sana ya kujenga majengo ya sekondari kwenye shule nyingi sana hapa nchini. Katika Jimbo langu la Bunda kuna shule nane, zina upungufu wa Walimu wa sayansi 56, na tunaposema walimu wa sayansi maana yake tuna masomo ya baiolojia, fizikia, kemia na hisabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, je, ni lini Walimu 56 wa sayansi watapelekwa katika Shule za Sekondari za Hunyari, Chamuriho, Mihingo, Mekomariro, Salama, Esparento, Makongoro, Nyamang’uta; ni lini hawa Walimu 56 watakwenda huko? Tunapouliza maswali haya maana yake ni kwamba watoto wako darasani, lakini Walimu wa sayansi hawapo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa Walimu wa sayansi bado ni changamoto ambayo Serikali tunaitambua na tumeweka mkakati wa kuhakikisha katika ajira zetu tunaweka kwanza kipaumbele cha Walimu wa masomo ya sayansi. Katika zile ajira ambazo zimepita asilimia kubwa ya walimu walioajiriwa ni Walimu wa masomo ya sayansi. Hata hivyo, tumeweka mkakati pia kwenye ajira zinazofuata, walimu ambao wataajiriwa kwa kiasi kikubwa ni Walimu wa sayansi ili kuwezesha kupunguza pengo la upungufu wa Walimu wa sayansi katika shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Getere kwamba wakati wa ajira hizo Halmashauri yake ya Bunda na shule hizi alizozitaja zitapewa kipaumbele kupata Walimu hawa wa sayansi ili kupunguza pengo la Walimu 56 ambao hawapo katika halmashauri hiyo. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali Wilaya ya Bunda inaishi karibu sana na Ziwa Victoria na Jimbo la Bunda ni kilometa 45 kutoka Ziwa Victoria. Sasa kwa sababu kuna pressure kubwa ya uvuvi wa samaki na kwa sababu sasa tunataka kupunguza hiyo pressure ya wavuvi wa samaki.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuweka mikakati ya kuweka vizimba katika Jimbo la Bunda na hasa pale kwenye mabwawa ya kuchimbwa kwa ajili ya kufuga samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni mkakati endelevu tulionao wa kuhakikisha kwamba tunakwenda kwenye eneo hili la ufugaji wa samaki na hasa upande wa Ziwa Victoria ambako kuna ufugaji wa kutumia vizimba na hivyo Jimbo la Bunda nalo litafikiwa.
MHE. MWITA B. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ningependa kujua Barabara ya Bariri – Mgeta, ambayo ahadi yake ilitolewa na Mheshimiwa Rais, mwezi wa pili mwaka huu, ni lini itamaliza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE):
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Bunda – Mgeta kama alivyoisema, iliahidiwa na viongozi na sisi kama Wizara pamoja na Serikali tunaendelea kutafuta fedha ili kutimiza hiyo ahadi ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunajua usalama ulivyo, Kituo cha Polisi Mgeta ni kituo kiko Makao Makuu ya Tarafa ya Chamuriho, toka mwaka jana nimeahidiwa kwamba fedha zitakwenda kumalizia boma la kituo hicho Waziri wa Mambo ya Ndani alishaahidi, wewe Naibu Waziri ulishaahidi. Je, ni lini hela zitakwenda kwenye kituo hicho?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumjibu Mheshimiwa Getere kwamba ni kweli kwamba kwa mara kadhaa tumeahidi kwamba kituo hicho kitakamilishwa na ndiyo tumeanza tu Mheshimiwa Getere, ni mwezi wa tatu tangu tulipoanza utekelezaji wa bajeti, ninakuahidi tu katika robo inayokuja tutahakikisha kupitia Jeshi la Polisi fedha inapelekwa ili kukamilisha ujenzi wa kituo cha Mgeta ambacho ni muhimu sana kwa usalama wa wananchi wa eneo la Mgeta na Tarafa nzima ya Wilaya ya Bunda Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru.(Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni miaka mingi sasa toka ukoloni vijana wetu wanaoajiriwa na Jeshi la Kujenga Taifa wanapewa miaka Sita kabla ya kuolewa au kuoa. Kwa kuwa, magonjwa yamekuwa mengi na kwa kuwa stress za Askari wetu zimekuwa nyingi.

Je, ni lini Serikali itapunguza muda huu wa miaka Sita kuwa miaka Mitatu au Miwil?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni muda sasa tunapeleka vijana wetu JKT tunapeleka vijana 2,000 au 1,000 wanachukuliwa labda 50 wanaajiriwa wengine wanarudi nyumbani. Je, ni lini sasa Serikali itakuja na mpango mkakati wa kuandaa vijana wanaorudi nyumbani kuwapa ufundi wa kutosha na saikolojia ili wasiwe panya road? (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Getere kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaanza kwa kumpongeza kwa kuwa mdau wa karibu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na kuwatetea wapiganaji wetu. Swali lake la kwanza ambalo ni kuhusu umri, napenda kwanza nitoe ufafanuzi kwamba ni kweli kwamba Maafisa na Maaskari wenye elimu ya darasa la saba hadi kidato cha sita na wenye Stashahada wao ndiyo hukaa miaka Sita kabla ya kuolewa. Yapo makundi mengine kama wenye shahada ya kwanza wao hukaa kama makapera kwa miaka Minne na wenye Shahada ya Uzamili, wao hukaa kwa miaka mitatu na wenye Shahada ya Uzamivu wenyewe hawana muda wa kukaa kwenye ukapera na hii ni kutokana na aina ya majukumu ambayo maaskari hawa wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Askari ambao nimewataja katika kundi la kwanza hao huwa ni vijana wadodo wanajiunga wakiwa na umri wa miaka 18 na kuendelea, kwa hiyo huhitaji kwanza kukomaa. Majukumu ya Jeshi ni majukumu mahususi lakini pia hawa ndiyo wanategemewa kama wapiganaji kwa hiyo huendelea na kozi mbalimbali na kuhakikisha kwamba wako imara wakati wote. Kwa hiyo, miaka hii Sita iliyowekwa imewekwa baada ya kufanya uchunguzi lakini pia kuzingatia vigezo mbalimbali. Kwa hiyo, kama tunaweza kubadilisha sidhani kama hilo linawezekana kwa sasa kwa sababu utafiti ulifanyika na lazima iwe hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii pia inatokana na aina ya majukumu ambayo wanafanya. Wengine wanapoajiriwa kama Madaktari huenda moja kwa moja kufanya hiyo kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ambalo linahusiana na vijana wanaokwenda JKT kwamba ni wengi lakini wanaoajiriwa ni wachache. Kwanza ninapenda kueleza kwamba madhumuni ya vijana kujiunga na JKT ni kuwajengea uzalendo, kuwajengea ukakamamu lakini kuwapa stadi mbalimbali ili baada ya hapo waende kujiajiri. Madhumuni siyo kutoa ajira kwa vijana hawa, hilo linafanyika vijana hawa wanafundishwa stadi mbalimbali ili baada ya hapo waweze kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu tuna mpango gani, ni kweli nasi tumeona kwamba pamoja na kuwapa stadi mbalimbali bado kuna umuhimu kuwawezesha vijana hawa kujitegemea. Kwa hiyo, tumeanza kufanya kazi hii na tayari katika mpango wa block farming kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, tutaona jinsi gani tutaweza kuchukua baadhi ya vijana, lakini bado tunaendelea kulichakata suala hili tuweze kuja na program nzuri zaidi ambazo zitawawezesha vijana hawa kujiajiri baada ya kupata stadi ambazo tunawapatia. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Naomba kujua, je, gari la wagonjwa lililoahidiwa kwenye Kituo Cha Afya Mgeta litaenda lini kwenye kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Boniphace Mwita Getere Mbunge wa Jimbo la Bunda Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kata aliyoitaja na uhitaji wa kituo cha afya hicho tutakwenda kuona uwezekano wa kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho kama kitakidhi vigezo tulivyoweka kwa ajili ya vituo vya afya vya Kimkakati ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Mchakato wa kupeleka barabara za TARURA, kutoka TARURA kwenda TANROADS ni barabara ya kutoka Bukama – Mikulusanga – Mikomalilo tulishafanya mchakato na umekamilika. Sasa hoja ya kujiuliza ni kwamba TANROADS na TARURA wakitaka kupeleka barabara, vigezo vya kuwapelekea TANROADS wanasema sisi mpaka tupelekewe na Wizara. Sasa ni lini muunganiko huu wa TARURA na TANROADS utakuwepo ili barabara za TARURA ziondoke kwenye TARURA ziende TANROADS?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna muunganiko mzuri kati ya TANROADS na TARURA na tunafanya kazi kwa kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, kinachofanyika tu ni kwamba kwenye zile barabara ambazo ziko chini yetu, huwa tunazipeleka kwao na wao wanaangalia vile vigezo vinavyostahili. Kwa hiyo, siyo kwamba wana nia ya kuchelewesha hizo barabara, ni kwa sababu wanaangalia vile vigezo, vikashakamilika wanatafuta fedha na ndiyo wanatangaza hizo barabara na kuwa za mkoa.

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kuimarisha ushirikiano wetu ili haya maswali ya Waheshimiwa Wabunge tuweze kuyajibu kwa wakati na kwa urahisi zaidi. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Naishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Miezi michache iliyopita Waziri wake alifika kwenye Jimbo langu akaangalia hatari kubwa ya lambo la Salamakati ambalo bado kidogo sana kutoweka. Kutokana na mvua zilizonyesha, lambo lile lina hatari kubwa sana ya kubomoka lote. Mheshimiwa Waziri aliahidi kuweka mikakati ya dharura ya kuziba lile lambo kabla halijabomoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupata majibu kuna mikakati gani ya kuziba lambo la Salama ambalo liko hatarini kubomoka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Naibu Waziri anaweza kunieleza nini kuhusu namna gani anaweza kwenda kuziba hilo lambo au kulijenga upya au kuliziba ile nyufa inayotaka kubomoka?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza tumepokea shukrani kutoka kwa Mheshimiwa Boniphace Getere. Pili ni juu ya ukarabati wa hili lambo. Naomba nilichukue jambo hili na kwenda kulisukuma ili liweze kufanyika sawa na ahadi ya Mheshimiwa Waziri.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Bariri kwenda Hunyali na kwenda mpaka Mgeta ni barabara ambayo iko kwenye barabara inayotoka Mwanza kwenda Musoma na barabara inayokwenda Serengeti. Kipande hicho cha barabara Mheshimiwa Rais Samia alipokuwa Bunda tuliomba kwamba kipande hiki kijengwe kwa kiwango cha lami. Ni lini barabara hii itajengwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hii ni ahadi ya Rais, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara inaendelea kuifanyia kazi ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami kama Mheshimiwa alivyokuwa ameahidi. Kwa sababu hayo sisi kwetu ni maelekezo na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutatekeleza kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; naomba kupata maelezo, Hospitali ya Wilaya ya Bunda tumepokea shilingi 3,650,000,000 na haina dalili za kumalizika, na Mheshimiwa Naibu Waziri ulikuja juzi ukaiona. Ni lini itamalizika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imepeleka zaidi ya shilingi 3,200,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Bunda; na wiki mbili zilizopita nilifanya ziara katika Halmashauri hiyo pamoja na Mbunge. Tulikubaliana, kwanza tunachukua hatua za kinidhamu kwa wataalam wote waliosimamia hospitali ile na kupelekea kutokukamilika kwa majengo ilhali fedha zilishapelekwa.

Pili, tumekubaliana kwamba fedha itapelekwa ili ikamilishe majengo yale mapema iwezekanavyo na huduma za afya zianze kutolewa, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pia nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, napenda kupata ufafanuzi, mwaka 1974 mpaka 1980 kulikuwa na program ya Serikali kupitia Wizara ya Mifugo ya kuwasaidia wanakijiji wa Kijiji cha Mekomariro kunenepesha mifugo yao, na baada ya miaka hiyo Serikali ikaacha maeneo hayo. Ni miaka 43 sasa maeneo hayo yanatumiwa na wanakijiji, na eneo lililokuwa linatumiwa na Wizara ya Mifugo halina hati wala halina GN. Ni kwa nini sasa wananchi wenye maeneo hayo bado wanasumbuliwa na Serikali kwamba eneo hilo ni la Serikali?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuna maeneo ya migogoro ya Mekomariro, Sirorisimba na Lemololi Mahanga, Ng’oroli na Mahanga, ni lini Serikali itaenda kuwasaidia maeneo hayo kuyapima na kuyapa hati za kimila? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili yaliyoulizwa na Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la shamba la kule Mekomariro ambalo linaonekana halina hati, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo halina ukweli wowote kwa sababu shamba lile tunavyofahamu Serikali, linayo hati. Ila tunatambua ukweli kwamba upo mgogoro baina ya shamba hilo na wananchi katika maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali la pili juu ya lini sasa Serikali itaenda kumaliza jambo hilo? Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya kumaliza kujibu maswali hapa, tutakaa mimi na yeye sasa tukubaliane ni lini twende katika eneo hilo ili kumaliza yale ambayo yanaendelea kuleta mgogoro katika eneo hilo.
MHE. BONIPHACE M. GETERERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, nina swali moja tu la nyongeza. Kwa kuwa kumekuwepo na maeneo mengi hapa nchini yaliyokosa sifa ya kuwa hifadhi na yamekuwa na migogoro mikubwa sana na wananchi. Ni lini Serikali sasa itafanya tathmini ya maeneo yote haya na kuyaleta hapa ili tuyagawe kwa wananchi, yote yaliyokosa sifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na maeneo mengi ambayo yamekuwa hifadhi kwa muda mrefu, lakini baadhi ya maeneo yamekuwa na changamoto ya migogoro kati ya wananchi pia na mamlaka za hifadhi.

Nimhakikishie kwamba Serikali inatambua changamoto katika maeneo hayo na tathmini inafanyika kwa kuzingatia sheria, taratibu na miongozo ya maeneo ya hifadhi ili kuhakikisha yale ambayo yanaendelea kukidhi sifa za kuwa maeneo ya hifadhi yaendelee kuwa maeneo ya hifadhi lakini yale ambayo yamepoteza sifa, Serikali inachukua hatua za kuendelea kuwapatia wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili tunalifanyia kazi ikiwemo la msitu huu ambao tumeujibia. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, nawapongeza Wizara ya Maji, wanafanya kazi vizuri sana; na waendelee kufanya hivyo hivyo.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Kwa kuwa huu mradi wa maji wa Ziwa Victoria kutoka Bunda Mjini kwenda Bunda Vijijini ni wa muda mrefu sana na una baraka zote za Waziri wa kwanza na Waziri aliyepo sasa hivi Mama Samia Suluhu Hassan, sasa Wizara ipo tayari kuweka mchakato wa single source ili kumpata mkandarasi wa haraka zaidi wa kutekeleza mradi huu?

Mheshimiwa Spika swali la pili; kwa kuwa tuna miradi kichechefu katika vijiji vya Kata ya Nyamswa; vijiji vya Makongoro A, Makongoro B, na Bukama na Vijiji vya Mgeta na Nyang’aranga; sasa ni lini Waziri atafika eneo hilo kusikiliza kero za wananchi kwenye miradi mibovu ya siku nyingi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili Mheshimiwa Gitere kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kupokea pongezi zake. Niseme, tuendelee kushirikiana. Lengo ni kuona tunafikisha maji safi na salama kwa wananchi na kuwatua akina mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Bunda Mjini kuelekea vijijini kutumia single sources; nimepokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge kwa sababu lazima tuajiri mhandisi mshauri ili aweze kutufanyia upembuzi yakinifu na kutuandalia maandalio ya kazi. Baada ya kumpata Mheshimiwa Mbunge wazo lako tutalifanyia kazi kwa kulipa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, kuhusu miradi chefuchefu, ni lengo la Wizara kuimaliza miradi chefuchefu yote, hivyo kufika kwenye maeneo ambayo bado maji ni tatizo ni moja ya majukumu yangu nikuombe Mheshimiwa Mbunge, mara baada ya Bunge hili la bajeti, mwezi wa saba tutaona namna njema ya kufika maeneo yote ambayo yanamiradi ambayo haifanyi vizuri.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kuna mradi wa densification na huu mradi ulikuwa unapeleka umeme kwenye Kitongoji cha Guta A, Gogea Mgeta, Bukoba Mgeta, Chamrio Mgeta, Tariamang’ari Kumsanga. Huu mradi wa densification ambao umekuwepo kwa muda mrefu, kasi yake ya kufanya kazi kwenye maeneo hayo imekuwa ni kidogo sana. Ni lini sana hivi vitongoji maalum ambavyo vina miradi mingi vitapata umeme wa densification?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Getere Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu maneno aliyoyataja ni mahsusi kwa mradi mahsusi basi ningependa baada ya hapa tuzungumze naye na wataalam wangu ili kuona changamoto mahususi katika eneo hilo ni zipi na tuweze kusaidia kuzitatua. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Je, ni lini Serikali kwa kuwa mchakato wa kupata Halmashauri ya Bunda ulishatekelezwa na tulishaandika, sasa ni lini Halmashauri ya Jimbo la Bunda itapata Halmashauri kutokana na umbali wa kutoka kwenye Jimbo langu kwenda kwenye Jimbo lingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Getere, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, michakato kufika TAMISEMI yote tunaikusanya na kama nilivyoeleza hapo awali bado kwa sasa kipaumbele kikubwa cha Serikali ni kuhakikisha tunakamilisha miundombinu katika Halmashauri ambazo zilikuwa ni mpya na Wilaya ambazo ni mpya, baada ya hapo sasa tutaanza kuangalia tena haya maeneo mengine ambayo Mikoa imepitisha na kuleta kwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais TAMISEMI.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kama inavyoonesha, kwamba kila mwaka na kila muda tunalipa Deni la Taifa ni kwa nini sasa Deni la Taifa halioneshi dalili ya kupungua ilhali kila mwaka tunalipa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini sasa Serikali italeta mchanganuo wa madeni yote tunayodaiwa kama nchi ili Wabunge tupate fursa ya kushauri katika ulipaji wa madeni hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza miradi ya kimkakati iliyo mikubwa nchini kwetu. Tunarejesha fedha lakini tuna uhitaji mkubwa tunaendelea kukopa.

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la pili, Serikali inawasilisha taarifa ya madeni yake kwenye Kamati ya Bajeti kila mwaka na kila inapohitajika. Tunaishukuru sana Kamati ya Bajeti kwa miongozo yake inayotusaidia kuendelea kufanya deni letu kuwa himilivu, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujua kwenye mwaka uliopita, katika bajeti Naibu Waziri, aliahidi kujenga barabara ya Bariri – Mgeta; je, sasa iko kwenye bajeti inayokuja?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, barabara hii amekuwa anaifuatilia; na kwa kuwa bado hatujapitisha bajeti, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira tuone kama hii barabara tumeshaipangia bajeti. Mpango wa Serikali ni kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; je, ni lini sasa Serikali itaimarisha Shule za Msingi Salakwa, Salama A na Salama B, Salama na Nyarubundu; ni lini majengo ya shule hizi yamezeeka sana, ya muda mrefu, lini Serikali itatekeleza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba baada ya session hii ya maswali nikae na Mheshimiwa Getere kuweza kuona ni hatua gani tunaweza tukazichukua za haraka kuweza kuzifanyia shule hizi matengenezo ambayo zinahitaji.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri nawashukuru sana Wizara ya Nishati, mmeleta pale vijiji 33 kutengeneza umeme kilometa mbili mpaka kilomita tatu na sasa Mkamburo Mkandarasi atengeneze kilometa moja tu na ameleta mzozo mkubwa kwa wananchi wale waliyopimiwa mara ya kwanza kuwaonyesha kwamba ni kilomita mbili. Ni lini sasa mtaongeza hizo kilomita mbili au tatu zilizokuwa zimepungua kutoka kilometa tatu mlizokuwa mmeongeza zamani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tunaendelea kukamilisha mikataba ya kuongeza kilomita mbili kwa kila kijiji kutoka kwenye ile kilomita moja ambayo ilikuwa inafanyika katika ya awamu ya tatu mzunguko wa pili wa REA.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku siyo nyingi wakandarasi wale ambao wameonekana wakikidhi kufanya vizuri miradi hii ya REA three round two watakuja site kuonyeshwa hizo kazi za nyongeza. Wale ambao wameonekana wakilegalega tutahakikisha tunapata wengine ili waje wafanye hiyo kazi na kuikamilisha yote kwa pamoja.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante naomba tu kujua Serikali itaenda lini kuangalia skimu ya umwagiliaji ya Kisango na skimu ya umwagiliaji ya Mariwanda ili kuifanyia kazi. Lini mtaenda kuangalia skimu hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha skimu zote zinafanyakazi ili tuongeze eneo la kilimo cha umwagiliaji. Nataka nimuhaidi Mheshimiwa Mbunge, kwamba nitawaelekeza watalamu wangu kwenda kupitia maeneo ambayo ameyataja ili tuweze kupata picha halisi na tuingize kwenye mpango. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nilikuwa nataka niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza; kwa kuwa hawa Madiwani kwa muda mrefu sasa na hasa sisi wa Chama cha Mapinduzi wakati tunapokuwa kwenye kampeni za uchaguzi huwa tunasema kuna mafiga matatu kwa maana ya Madiwani, Wabunge na Rais na wao ndio wanaosimamia miradi ya Serikali. Sasa hatuoni kuna haja kwa kweli ya kuwaongeza kiasi fulani angalau kutoka kwenye eneo walipo ili kufika eneo wanalolitaka wao kwa sababu eneo ni kidogo sana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; hawa Madiwani kwa muda mrefu sasa huko nyuma wengi wamechaguliwa na hawapati mafunzo ya Serikali. Lini sasa Serikali itaandaa mafunzo kwa Madiwani ili na wenyewe wawe na uelewa wa kusimamia miradi yetu katika maeneo yetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la kwanza la nyongeza la kuhusu kuongeza posho hizi za Madiwani, Serikali itafanya tathimini na kuangalia ni namna gani hili linaweza likatekelezeka kulingana na bajeti ambayo Serikali inayo. Kwa sbabu haya mambo yanahusisha ongezeko la matumizi kwa Serikali. Tayari kama ambavyo mnafahamu Waheshimiwa Wabunge wote humu ndani kwamba mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali ilichukua jukumu kutoka kwenye halmashauri zote la kulipa hizi posho kwa mwezi zilienda Serikali Kuu. Kwa hiyo, tutaliangalia na lenyewe na kuona kama uwezo wa Serikali utauhusu kwenye bajeti zijazo tuweze kulichukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye swali la pili la mafunzo kwa Madiwani; hili liko kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zenyewe. Kuna halmashauri ambazo zinatoa maunzo haya kwa kushirikisha Taasisi za Uongozi Institute, kwa kushirikisha Taasisi kama Chuo cha Utumishi wa Umma. Kwa hiyo, niwatake wakurugenzi katika halmashauri mbalimbali nchini kuhakikisha wanatenga bajeti ya kutoa mafunzo kwa Madiwani wa halmashauri zao.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba kujua katika bajeti ya mwaka 2022/2023, Serikali iliahidi kupeleka maji ya Ziwa Victoria katika Jimbo la Bunda. Je, ni lini ahadi hii itatimizwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tayari mradi ambao unatarajiwa kupelekwa Bunda umefikia hatua nzuri, Mhandisi
Mshauri yuko site. Mheshimiwa Mbunge nakupongeza kwa kufuatilia, kama tulivyoongea wiki iliyopita ofisini, tayari Mhandisi Mshauri anakamilisha na wiki hii tunamtarajia arejeshe taarifa ya kuona tathmini ya thamani ya mradi ambao tutakwenda kuujenga.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Hili suala la upande wa Zanzibar kupata pensheni ya wazee wote na Tanzania Bara kukosa wakati ni nchi moja, naomba kujua, nini tamko la Serikali kuhusu wazee wa Bara ambao wanatakiwa kupata pensheni sawa na wazee wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kama nilivyojibu kwenye swali la msingi kwamba kwenye masuala ya kipensheni tayari tunayo Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, kwa hiyo mtu yeyote kwa sasa, hata kabla ya uzee, unaweza ukaanza kupeleka fedha.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa pili, kuhusiana na kwamba tutoe tamko; ni hilo la kufanya utafiti ili kuweza kujiridhisha uwezo wa Serikali katika kuhudumia wazee hawa.

Mheshimiwa Spika, tatu, suala hili tayari wazee wanahudumiwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa sasa tunavyo vituo 14 vya wazee wasiojiweza ambavyo ni vya Serikali, vinahudumia hawa wazee na vituo 15 vya watu binafsi na jumla ya wazee 496 wanapata huduma kwenye hayo maeneo.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Serikali ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, iliweka mpango wa TASAF ambao unanufaisha wazee. Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imeona bado pia kuna umuhimu wa kuwahudumia wazee, imeweka utaratibu wa mikopo, utoaji wa fursa na mitaji; Serikali hii hii imeweza kuendelea kuwaangalia wazee kwa kuwatolea huduma ya matibabu bure na kuna desks zaidi ya 588 kwenye hospitali zetu kwa ajili ya kuwahudumia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili suala Serikali inaliangalia kwa kina sana kuona namna gani wazee wetu tunawaenzi na kuwaheshimu katika mchango mkubwa walioutoa wakati wa ujana wao kuchangia uchumi wa Taifa. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, katika maswali ya kuangalia sana ni hili swali. Tumeona Serikali ikiwa ikivamia wananchi kwenye maeneo yaliyovamiwa na Serikali wanabomolewa nyumba zao. Miaka 14 sasa wananchi takriban nchi nzima maeneo yale ambayo ni maeneo nyeti ya barabarani yamekaliwa na Serikali bila fidia, bila kwenda kuyapima. Sasa swali langu lilikuwa linahusu;

Je, ni lini Serikali itatoa tamko la wananchi kung’oa vila vigingi na kuingia kufanya maeneo hayo kwa shughuli za maendeleo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali imesema kwamba maeneo ambayo yamechukuliwa toka 2009 mpaka leo, kuna mengine yatafidiwa kuna mengine kuna hayatafidiwa;

Je, wale ambao hawatafidiwa wako tayari kupewa hela ya usumbufu, kwa maana ya fidia ya usumbufu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, baada ya kuliona hili tatizo katika bajeti ambayo tumepitishiwa ya mwaka huu wa 2023/2024 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kufanya tathmini, na hili linapatikana kwenye ukurasa wa 194 wa kitabu chetu. Tumeeleza hili suala na changamoto yake ambayo ipo. Na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba wale ambao wako ndani ya mita 7.5 nyumba zao hazijabomolewa; ila ziliwekwa alama ya X ya kijani ikionyesha kwamba barabara imewafuata na wanastahili fidia. Kwa hiyo kwa sababu ya nchi nzima ndiyo maana Serikali imekuja kufanya tathmini ione ni maeneo yapi ambayo kweli sasa tutayahitaji na yatafidiwa, na yale ambayo hatutahitaji kwa sasa wananchi wataruhusiwa waendelee kuyatumia baada ya kufanya hiyo tathmini.

Mheshimiwa Spika, hao wa usumbufu nadhani sheria zetu na kanuni zetu za namna ya fidia inavyofanyika zitatumika ili kuona namna ya kuwafidia wale ambao watakuwa wamepata huo usumbufu, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda kuuliza, hivi ni lini Serikali itaamua kutengeneza mikataba ya Kiswahili katika utengenezaji wa barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, hili la Mheshimiwa Getere, niseme tunalichukua na tutaangalia ni namna gani tunaweza tukaboresha na kuwa na mikataba ya Kiswahili.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hii Wizara ndiyo inahusika na masuala ya TASAF watu wangu wa Jimbo la Bunda kumekuwa na matatizo makubwa sana ya malipo ya TASAF karibu nchi nzima, naomba Waziri atamke kwamba kuna nini kinachoendelea katika TASAF?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Getere, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Getere najua swali lake linatokana na ukweli kwamba yako baadhi ya matatizo au changamoto zilizojitokeza katika utendaji ndani ya Taasisi yetu inayosimamia Mfuko wa Kunusuru Kaya Maskini yaani TASAF.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba yako maamuzi na maelekezo makubwa yaliyokwishafanyika ambayo sasa yale mapungufu yote yaliyojitokeza au mapungufu kwa asilimia kubwa yaliyojitokeza ndani ya TASAF tunaweka sawa. Nataka nimhakikishie kwamba yeye na Wabunge wote humu ndani wasiwe na wasiwasi Serikali iko kazini na kazi ya kurekebisha zile kasoro zote zinaendelea kufanyika, ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itajenga Sekondari mpya Kata ya Ketare eneo la Nyaburundu na Kata ya Mihingo eneo la Machimero kwa sababu ni muda mrefu Serikali imeahidi kujenga sekondari hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, lini Serikali itajenga sekondari mpya katika maeneo ambayo ameyataja Mheshimiwa Mbunge, kwa sasa Serikali inajenga shule mpya katika kila halmashauri hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwa Mheshimiwa Getere pia amepata zaidi ya shilingi milioni 580 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya na tutazidi kutafuta fedha kwa sababu Serikali hii ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele cha kuhakikisha kata zote ambazo hazina sekondari zinajengewa sekondari mpya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge avute subira tutakapomaliza ujenzi wa hii shule ya shilingi milioni 580 ambayo iko jimboni kwake tutaendendelea kutafuta fedha nyingine kwa ajili ya ujenzi wa shule za sekondari katika kata ambazo amezitaja.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ninaomba kujua Mheshimiwa Naibu Waziri umepita sana barabara ya Sanzati kwenda Nata. Sasa ni lini hiyo barabara itamalizika maana imekuwa kero kwa wananchi wa Bunda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nichukue nafasi hii kusema kwamba, Mkandarasi tayari yuko site anafanya kazi. Nawahimiza Watendaji wa TANROADS pamoja na Meneja wa Mkoa ambao wanamsimamia Mkandarasi, kuhakikisha kwamba wanamsimamia ili aongeze kasi na kukamilisha barabara hiyo ambayo inahitajika sana kwa wananchi wa Bunda pia wananchi wa Wilaya ya Serengeti.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza; je, ni lini Serikali itapeleka mtandao katika Vijiji vya Hunyali, Kihumbu na Sarakwa?

NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge tayari ameshafika ofisini kwetu na mimi nimekuwa nikiwasiliana naye mara kwa mara na tayari vijiji ambavyo ameshavileta ofisini viko kwenye mchakato wa kuingizwa katika utekelezaji. Pindi fedha zitakapopatikana tutafikisha huduma ya mawasiliano katika vijiji ambavyo Mheshimiwa Getere amevitaja.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Vijiji 33 vya Bunda vilipewa umeme kilomita tatu kwa kila kijiji na sasa Mkandarasi amepeleka kilomita moja kwa kila kijiji. Ni lini kilometa mbili zitaongzwa katika vijiji 33 vya Jimbo la Bunda?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze Wabunge wa Mkoa wa Mara kwamba katika zile lot ambazo Wakandarasi wao tayari wamekamilisha original scope kwa asilimia 100 na Mkandarasi wa Mkoa wa Mara tayari naye yumo katika orodha ile, kwa hiyo tuendelee kusukuma kwa pamoja ili tuweze kukamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatarajia mwishoni mwa wiki hii wanzetu wa REA watasaini mikataba na wale ambao wamepata nafasi ya kuongeza hizo kilomita mbili ambazo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa bilioni 351 kwa ajili ya kuongeza kilomita mbili kwa kila Kijiji. Tunatarajia wiki hii zitasainiwa na hivyo mwanzoni mwa mwezi unaokuja kazi za kusimika nguzo na kuvuta waya utaanza katika maeneo hayo ambayo nyongeza ya kilomita mbili inaenda kufanyika.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kujua, hivi karibuni kumekuwa na utata sana wa Bima ya Afya CHF kwa wananchi wa vijijini. Hii bima imefutwa au ipo? Nini tamko la Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, bima hii haijafutwa na tunashirikiana na wenzetu wa TAMISEMI ambao ndiyo wanasimamia eneo hili la CHF ili kuona katika kipindi hiki cha mpito ambacho kuna haya matatizo ambayo Wabunge mnayazungumzia tunaboreshaje pamoja sisi na TAMISEMI tuone ni namna gani tunaiboresha ili kuondoa matatizo yayosemwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo kuna wenzetu ambao wanafadhili eneo hili kuna Taasisi inafadhili eneo hili wanasaidia kwenye matangazo wanasaidia kwenye kuhamasisha, tunataka tukae nao pamoja tuone namna gani badala ya kufanya matangazo, kufanya warsha na tamasha warudishe hizo fedha waende kuboresha kwenye eneo la kitita ili wananchi kuweza kuondokana na tatizo hili. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Bunge lako lilitunga sheria ya kutoza faini ya boda boda shilingi 10,000 kwa kosa ambalo mwendesha boda boda amefanya. Siku hizi kumetokea matatizo, boda boda sasa hawatozwi faini ya shilingi 10,000, badala yake wanapelekwa Mahakamani kutozwa faini ya shilingi 30,000. Nini tamko la Serikali kuhusu jambo hili?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli hii faini anayoisema ya Shilingi 10,000/= ni ya papo kwa hapo, lakini wakati mwingine Polisi wanatathmini ukaidi na uzoefu wa hawa vijana kufanya makosa makubwa ya barabarani na hivyo huwapeleka Mahakamani ili Mahakama ambacho ndiyo chombo cha mwisho katika utoaji wa haki watoe hukumu kulingana na uzito au uzembe unaosababisha ajali.

Mheshimiwa Spika, kama amepelekwa Mahakamani na Mahakama imeamua vile, nadhani Mheshimiwa Mbunge tukubaliane. La muhimu ni kuwahimiza vijana wetu waepuke kufanya makosa wanayoweza kuyaepuka ambayo mengi yanasababisha ulemavu na vifo miongoni mwao, nashukuru.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na ninashukuru kwa majibu ya Serikali. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa sasa Serikali imetamka wazi kwamba mradi huu utaanza bajeti ijayo 2023/2024 sasa Serikali inaweza kuwaambia wananchi wa Bunda kwamba ni Bajeti kiasi gani imetengwa kwa mradi huo?

Swali la pili; kwa kuwa Serikali imetumia zaidi ya milioni 52 kufanya usanifu yakinifu kama kuchimba malambo ya Salama A, Lakana, Burundu, Kambugu, Tingirima na Mihingo. Je, ni lini miradi hii itakamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Getere kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na bajeti kwenye Jimbo la Bunda, Mheshimiwa Mbunge unafahamu na nikupongeze kwanza kwa ushirikiano wako ulifika Wizarani umeweza kukutana na Waziri na Katibu Mkuu. Yote hii ni jitihada ya kuona kwamba hili linafanyika. Kwa eneo lako la Bunda zaidi ya bilioni 1.7 imepangwa na itaenda kutumika kutokana na zile bilioni 750 kwenye ule mradi wa Ziwa Victoria kwako ni zaidi ya bilioni 1.7.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na uchimbaji na ukamilishaji wa haya mabwawa Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Waziri alishakuelekeza vizuri na tumshukuru zaidi Mheshimiwa Rais kwa kutupatia sisi Wizara ya Maji vifaa au vitendea kazi. Tumeshapata mitambo na huu mtambo mmojawapo wa kuchimba mabwawa unaletwa Bunda mahsusi kuhakikisha haya Mabwawa yanakwenda kuchimbwa na yanakamilika na Mheshimiwa Mbunge tutakuharifu tutakwenda pamoja kwa sababu tunashirikiana vizuri.
MHE.BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Jimbo la Bunda limekuwa na kituo cha muda mrefu cha zamani kinaitwa Ikizu, na kimechaka sana, na Serikali imetoa ahadi ya kukarabati vituo vya zamani vya afya;

Je, ni lini Kituo cha Ikizu kitakarabatiwa kwa ahadi ya Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakaa na Mheshimiwa Getere ili kuweza kuona ahadi hiyo ya Serikali ilitolewa lini ili tuweze kuifatilia vizuri kwenye idara husika ambayo ilitoa ahadi hiyo na tuweze kuhakikisha tunapata fedha kwa ajili ya kukarabati kituo cha afya hicho alichokitaja Mheshimiwa Getere.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, majibu ya Waziri yananipa wasiwasi, kwa sababu mimi nimekuwa Mjumbe wa Kamati ya Viwanda na inavyosemekana kwamba huyo mwekezaji wa kwanza ana matatizo na Serikali, inaonekana kwamba uwezo wake haupo. Sasa majibu ambayo anatupa Waziri ni ya Mkandarasi mwekezaji mpya au mwekezaji wa kwanza?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ni kweli Mkandarasi huyu baada ya kutokutekeleza mradi huu kwa wakati kulingana na mkataba ule wa awali, Serikali tuliweza kufanya ufuatiliaji wa uwezo wa mkandarasi huyu. Kweli katika moja ya vitu ambavyo vilionekana ni kwamba alikuwa na uwezo mdogo, lakini baada ya majadiliano ya hivi karibuni amesema anaweza kufanya lakini bado tunaendelea kuona kama kuna mwekezaji mwingine ambaye anaweza kuwekeza baada ya kumalizana na huyu aliyeko mwanzo kama atashindwa.

Mheshimiwa Spika, katika majadiliano haya mojawapo ni kuona na kutathmini uwezo wa mwekezaji huyu wa mwanzo Sichuan Hongda na tukiona kwamba hana uwezo kulingana na taarifa ambazo tumezipata na vyanzo vya kutoka nchini kwake then tunaweza kutafuta sasa mwekezaji mwingine kulingana na utaratibu wa mkataba wa awali ambao lazima tuuvunje au tutafute namna nyingine ili kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa manufaa ya nchi. Kwa hiyo, haya yote katika majadiliano haya ya sasa hivi yanazingatiwa. Nakushukuru sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa kata zote zilizotajwa hapo saba hazipo hata kata moja ambayo ipo kwenye Tarafa ya Chamriho; na kwa kuwa Tarafa ya Chamriho ina kata ya Nyamanguta, Nyamswa, Kitale, Salama, Bihingo, Mgeta na Unyali. Sasa ni lini Serikali itapeleka mradi huu ambao uko Bunda kwenye hizo kata alizotaja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa mradi huu unaelimisha watu juu ya madhara ya climatic change Serikali ina mkakati gani sasa wa kupeleka semina mbalimbali na warsha katika maeneo haya ili kuelimisha watu juu ya tabia nchi inayotokea kwenye maeneo haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu la msingi ukiangalia kwenye paragraph ya pili imeonesha kwamba Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, tunaendelea kufanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha kwamba tunakaa na wadau na wafadhili mbalimbali ili kuweza kupata fedha twende tukaendeleze mradi huo katika hiyo Tarafa ya Chamriho. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge aendelee kuwa na Subira, lakini pia kama kuna namna ya kufanya Halmashauri ya Wilaya ya Bunda watuandikie hilo andiko walilete kwetu Ofisi ya Makamu wa Rais, twende tukalipeleke kwa ajili ya kuliombea fedha ili tukakamilishe mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, miongoni mwa kazi yetu kubwa tunayoifanya katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuhifadhi mazingira ni kuchimba visima maeneo mbalimbali ili kunusuru hali hiyo. Kwa hiyo nimwambie tu kwamba tunakwenda kutafuta fedha ili twende tukachimbe visima ili kuweza angalau kuokoa maeneo hayo huku tukisubiria mradi huo uweze kukamilika. Nakushukuru.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nipongeze majibu mazuri sana ya Naibu Waziri. Hata hivyo, kwa heshima ya Mheshimiwa Boniphace Getere na nikifahamu kwamba ameendelea kuwapambania wananchi wake kwa nguvu kubwa sana. Ofisi yetu itafanya kila liwezekanalo mwanzoni mwa mwaka wa fedha katika eneo hilo tutatengeneza borehole moja ya mfano kama kuwafariji wananchi wa Kata ya Chamriho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sambamba na maelekezo yaliyotolewa na Naibu Waziri katika majibu ya awali. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Getere kwamba, tutakwenda kuchimba borehole ya haraka sana katika Kata ya Chamriho. Lengo letu ni kuanzia hapo kwanza wakati tukijadili mambo mengine, ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza na naishukuru Serikali kwa Wizara ya Ujenzi kwa kuhangaika na ujenzi wa lami kwa barabara ya Bariri - Mgeta. Sasa kwa sababu mmekwishafanya upembuzi yakinifu na mmeshafanya tathimini ya ujenzi; ni lini sasa hii barabara ya Mgeta - Bariri itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Bariri - Mgeta ni barabara ambayo inasimamiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha ili ikishapata fedha basi hii barabara ambayo ni njia ya mkato kwenda Nata - Mgumu iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na ninamshukuru Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza:

Mheshimiwa Spika, kwanza; kwa kuwa sasa tuna elimu bure ya sekondari na mpaka Kidato cha Sita. Ninashukuru kwa hilo kwa Serikali, nimshukuru Mama Samia kwa kutoa elimu bure kwa Kidato cha Tano na cha Sita. Sasa lipi Serikali itafanya kusamehe michango ya sekondari 20,000? Kusamehe michango ya Kidato cha Sita na cha Tano ya 70,000 au kutoa michango ya sekondari ambayo inafikia Shilingi Laki Tano au michango ya Kidato cha Sita ambayo inafikia Shilingi Milioni Moja, kipi kifanyike sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa swali lake lilikuwa ni la jumla na nimwambie tu kwamba baada ya elimu bila ada maana yake wanafunzi wale hawalipi ile ada ambayo walikuwa wanalipa ya Shilingi 20,000 kwa Kidato cha Kwanza mpaka cha Nne. Maana yake na hivi tunavyokwenda kwa Kidato cha Tano na Kidato cha Sita ambapo ada kwa miaka yote imekuwa ni Shilingi 70,000 maana yake sasa hivi wazazi hawatalipa hiyo ada ya Shilingi 70,000. Kwa hiyo, huo ndiyo msimamo wa Serikali kuhakikisha kwamba tunawasaidia wananchi wote wa Tanzania ili waweze kupata elimu bila malipo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu hiyo michango mingine tunaendelea kuiangalia ili kuhakikisha kwamba haiathiri masomo ya wanafunzi na wazazi kuhakikisha watoto hawa wanapata elimu bora. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka kujua Kituo cha Afya Honyali, tulikipelekea shilingi milioni 250 wajenge na baada ya hapo wataongeza milioni 250 kukimalizia. Wananchi wamejitahidi kwa kupitia Halmashauri ya Bunda na wako katika hatua nzuri. Ni lini sasa hela ya pili itaenda shilingi milioni 250 ili wamalizie kituo chao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tulipeleka shilingi milioni 250 na kazi ya Ujenzi wa Kituo cha Afya inakwenda lakini masharti ni kwamba baada ya kukamilisha ujenzi wa shilingi milioni 250 ndipo shilingi milioni 250 nyingine zitapelekwa. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba tutapeleka mara baada ya kukamilisha matumizi ya shilingi milioni 250 ya kwanza. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Hospitali ya Makambako imeshapata X-ray na Ultrasound naomba kuuliza swali moja tu la nyongeza; Kituo cha Afya Ikizu kina muda mrefu sana tukiwa na maombi ya X-ray na mwaka jana walisema wangepata lakini hawajapata. Ni lini sasa Kituo cha Afya Ikizu kitapata X-ray?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vyetu vya afya vingi havina mashine za X-ray, lakini bado tutaangalia vigezo ambavyo vitapelekea baadhi ya vituo kupata kipaumbele kuliko vituo vingine, kwa hiyo, naomba nichukue hiki Kituo cha Afya cha Ikizu ili tukafanye upembuzi na kuona uhitaji wa X-ray lakini baada ya hapo tutatafuta X-ray kwa ajili ya kituo hicho pia, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni miaka mitatu sasa toka wananchi wa Tarafa ya Chamriho wameahidiwa kujengewa VETA na wameshatoa eneo bure ekari 55. Ni lini sasa hiyo VETA ya Tarafa ya Chamriho itajengwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa juhudi za wananchi za kutenga eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha VETA. Lakini nimuondoe wasiwasi na niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge wote ambao maeneo yao bado Vyuo vya VETA vya Wilaya havijajengwa, katika mwaka wa fedha ujao dhamira ya Serikali kama ilivyo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, lakini kama ilivyo kwenye Sera kwamba tunakwende kujenga Chuo cha VETA katika kila Wilaya ikiwemo na Wilaya hii ya Mheshimiwa Getere katika mwaka ujao wa fedha tunaamini kabisa tutaweza kuanza ujenzi katika eneo hili. Nakushukuru.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na ninamshukuru Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza:

Mheshimiwa Spika, kwanza; kwa kuwa sasa tuna elimu bure ya sekondari na mpaka Kidato cha Sita. Ninashukuru kwa hilo kwa Serikali, nimshukuru Mama Samia kwa kutoa elimu bure kwa Kidato cha Tano na cha Sita. Sasa lipi Serikali itafanya kusamehe michango ya sekondari 20,000? Kusamehe michango ya Kidato cha Sita na cha Tano ya 70,000 au kutoa michango ya sekondari ambayo inafikia Shilingi Laki Tano au michango ya Kidato cha Sita ambayo inafikia Shilingi Milioni Moja, kipi kifanyike sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa swali lake lilikuwa ni la jumla na nimwambie tu kwamba baada ya elimu bila ada maana yake wanafunzi wale hawalipi ile ada ambayo walikuwa wanalipa ya Shilingi 20,000 kwa Kidato cha Kwanza mpaka cha Nne. Maana yake na hivi tunavyokwenda kwa Kidato cha Tano na Kidato cha Sita ambapo ada kwa miaka yote imekuwa ni Shilingi 70,000 maana yake sasa hivi wazazi hawatalipa hiyo ada ya Shilingi 70,000. Kwa hiyo, huo ndiyo msimamo wa Serikali kuhakikisha kwamba tunawasaidia wananchi wote wa Tanzania ili waweze kupata elimu bila malipo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu hiyo michango mingine tunaendelea kuiangalia ili kuhakikisha kwamba haiathiri masomo ya wanafunzi na wazazi kuhakikisha watoto hawa wanapata elimu bora. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. Ningependa kujua Halmashauri ya Bunda ina Majimbo mawili ambayo Halmashauri moja ipo Jimbo la Mwibara lakini Majimbo hayakutani, yamekatwa katikati na Jimbo la Bunda Mjini. Ni lini sasa Serikali itapeleka Halmashauri ya Nyamswa kwenye Jimbo la Bunda Vijijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniface Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu maombi ya kuanzisha mamlaka mpya kwa maana ya Halmashauri ya Nyamswa, nimuombe Mheshimiwa Mbunge lakini nimuelekeze Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bunda, kuanza taratibu ambazo ziko kwa mujibu wa Sheria Sura 288 na kuwasilisha Ofisi ya Rais TAMISEMI ili tuweze kufanya tathmini ya vigezo hivyo. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ni lini atapeleka fedha katika Zahanati ya Tiling’ati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba ni kweli Zahanati ya Tiling’ati tulifika pale na wanahitaji shilingi milioni kumi kwa ajili ya ukamilishaji na Mheshimiwa Waziri wa Nchi alishaahidi kwamba fedha zitakwenda pale. Namhakikishia kwamba tutafuatilia kuhakikisha kwamba shilingi milioni kumi zinapelekwa pale Zahanati ya Tiling’ati, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kuna majibu mengine yanasikitisha sana. Kituo cha Mugeta kimeisha mwaka 2019, wakati kituo hiki tunajenga tulipewa shilingi milioni 700, siyo kwamba hela zinatafutwa hapana, shilingi milioni 700, shilingi milioni 400 wakasema tujenge majengo kwa kushirikiana na wananchi na shilingi milioni 300 zinaenda MSD vifaatiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipoenda kufuatilia mwaka 2020 tukaambiwa vifaatiba vitakuja vya shilingi milioni 161 na vimeshakuja. Wakasema vifaa vingine vya shilingi milioni 139 viko njiani, leo unaambiwa kuna bajeti inatengwa, hizi shilingi milioni 300 zilizoenda MSD ziko wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua tutatengaje bajeti ambayo tayari ilishaenda? Kwa hiyo, naomba hili jokofu la Mugeta lipelekwe, fedha zipo MSD. (Makofi)
Swali la pili, tumejenga Kituo cha Afya Hunyari lakini hakina theater, sasa naomba kujua ni lini hii theater ya Kituo cha Afya Hunyari itakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namwelewesha Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha za vifaatiba haimaanishi ni fedha za kununua jokofu la mochwari peke yeke. Tukikamilisha ujenzi wa kituo cha afya vifaatiba vya kipaumbele ni vifaa ambavyo vitakwenda kutibu wananchi. Vifaa vya upasuaji, vifaa vya wodini, vitanda, magodoro na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili tunakwenda kupeleka vifaa kwa ajili ya kuhifadhia maiti kwa maana ya majengo ya mochwari pamoja na majokofu. Kwa hiyo, hiyo shilingi milioni 300 ambayo ilikwenda MSD ilinunua vifaatiba ambavyo viliwezesha kituo cha afya hicho kuanza kutoa huduma kwa wananchi. Mwaka huu wa fedha tayari Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshawaletea shilingi milioni 700 kwa ajili ya kununua vifaatiba vingine likiwemo jokofu la mochwari. Naomba Mheshimiwa Mbunge tuishukuru Serikali kwamba imefanya kazi kubwa, imeleta fedha nyingi za vifaatiba, jokofu litanunuliwa kati ya Februari na Machi ili wananchi wa Bunda waweze kupata huduma nzuri za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kuhusu Kituo cha Afya cha Hunyari ni kweli kwamba kuna majengo ambayo yamejengwa lakini bado hatuna jengo la upasuaji. Safari ni hatua, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa awamu ili twende kukamilisha majengo mengine kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Hunyari. Ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba tu nijazilize hapo alipoongelea Mbunge aliyemaliza kuongea. Mtu mwenye sifa za kupiga kura za Urais ni raia wa Tanzania mwenye uraia wa Tanzania mwenye sifa za kupiga kura, maana yake ni raia amejiandikisha, ana umri wa miaka 18, ni raia wa Tanzania; sasa kama hao wana sifa za kupiga kura za Rais wametambulika kwamba ni Watanzania, kwa nini hawachagui Diwani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge hizo ni sehemu ya sifa za mpiga kura lakini kama nilivyotangulia kusema, kuchagua viongozi ngazi ya vijiji vile na ngazi ya kata zile ambazo zina mchanganyiko mkubwa wa wakimbizi na watu ambao siyo raia kunahitaji umakini mkubwa ili kulinda usalama wa nchi na Serikali inaendelea kuchukua hatua ambazo zitawawezesha sasa kwenda kufanya uchaguzi huo baada ya kujiridhisha na mazingira ya kufanya chaguzi katika maeneo hayo, ahsante.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza na naishukuru Serikali kwa kuchimba Bwawa la Kihumbu. Sasa nataka kuuliza, kwa sababu bwawa limechukua muda mrefu kidogo pamoja na kwamba jitihada zipo.

Je, ni lini sasa hilo bwawa litakamilika ili wananchi watumie maji ya bwawa hilo na mifugo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli bwawa halijakamilika; Serikali tayari imeshakutana na mkandarasi na imeshampa deadline juu ya lini bwawa linatakiwa kukamilika na tayari tumeshakubaliana. Mara tu mkataba utakapokuwa umekamilika bwawa hilo litakuwa limekamilika na atatukabidhi Serikallini kwa ajili ya kuendelea kulitumia.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kuna majibu mengine yanasikitisha sana. Kituo cha Mugeta kimeisha mwaka 2019, wakati kituo hiki tunajenga tulipewa shilingi milioni 700, siyo kwamba hela zinatafutwa hapana, shilingi milioni 700, shilingi milioni 400 wakasema tujenge majengo kwa kushirikiana na wananchi na shilingi milioni 300 zinaenda MSD vifaatiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipoenda kufuatilia mwaka 2020 tukaambiwa vifaatiba vitakuja vya shilingi milioni 161 na vimeshakuja. Wakasema vifaa vingine vya shilingi milioni 139 viko njiani, leo unaambiwa kuna bajeti inatengwa, hizi shilingi milioni 300 zilizoenda MSD ziko wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua tutatengaje bajeti ambayo tayari ilishaenda? Kwa hiyo, naomba hili jokofu la Mugeta lipelekwe, fedha zipo MSD. (Makofi)
Swali la pili, tumejenga Kituo cha Afya Hunyari lakini hakina theater, sasa naomba kujua ni lini hii theater ya Kituo cha Afya Hunyari itakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namwelewesha Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha za vifaatiba haimaanishi ni fedha za kununua jokofu la mochwari peke yeke. Tukikamilisha ujenzi wa kituo cha afya vifaatiba vya kipaumbele ni vifaa ambavyo vitakwenda kutibu wananchi. Vifaa vya upasuaji, vifaa vya wodini, vitanda, magodoro na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili tunakwenda kupeleka vifaa kwa ajili ya kuhifadhia maiti kwa maana ya majengo ya mochwari pamoja na majokofu. Kwa hiyo, hiyo shilingi milioni 300 ambayo ilikwenda MSD ilinunua vifaatiba ambavyo viliwezesha kituo cha afya hicho kuanza kutoa huduma kwa wananchi. Mwaka huu wa fedha tayari Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshawaletea shilingi milioni 700 kwa ajili ya kununua vifaatiba vingine likiwemo jokofu la mochwari. Naomba Mheshimiwa Mbunge tuishukuru Serikali kwamba imefanya kazi kubwa, imeleta fedha nyingi za vifaatiba, jokofu litanunuliwa kati ya Februari na Machi ili wananchi wa Bunda waweze kupata huduma nzuri za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kuhusu Kituo cha Afya cha Hunyari ni kweli kwamba kuna majengo ambayo yamejengwa lakini bado hatuna jengo la upasuaji. Safari ni hatua, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa awamu ili twende kukamilisha majengo mengine kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Hunyari. Ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujua, lini wananchi wa Jimbo la Bunda watapata umeme wa REA II C kwa vijiji 147?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mradi wetu wa II C tumetenga vitongoji 17 na kwa mradi ujao pia, vitongoji 15 Jimbo la Bunda litapata. Kwa hiyo, kwa kuanzia wataanza na vitongoji 32, ahsante.