Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Ester Amos Bulaya (1 total)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Mheshimiwa Waziri Mkuu, mwaka 2018 tulipitisha Sheria ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na lengo kuu lilikuwa kuunganisha mifuko na vile vile kuhakikisha maslahi ya wafanyakazi yanaboreshwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kupitisha sheria hiyo, matarajio ya wafanyakazi hayakuzingatiwa na matokeo yake, Hayati John Pombe Magufuli alisitisha matumizi ya sheria ile. Mpaka sasa hivi baada ya kusitishwa, ongezeko la watumishi wanaostaafu kwa hiyari limeongezeka, ongezeko la fao la kujitoa limeongezeka na mifuko imekuwa ikilemewa kulipa mafao ya wastaafu kutokana na watu kutokujua hatima yao na kuamua kuwahi kustaafu kabla ya wakati.

Je, ni lini Serikali mtaleta mabadiliko ya sheria ambayo tayari mliji-commit zaidi ya mara tatu, hamkufanya hivyo; ili sasa wastaafu wetu wawe na uhakika wa maisha yao baada ya kustaafu kwamba yamezingatiwa kwenye sheria na kile walichokitaka? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bulaya, Mbunge wa Musoma… (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ni Mkoa wa Mara, siyo Musoma, maana nitakuwa na mgogoro na Mheshimiwa Mathayo. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri jambo hili liko Ofisi ya Waziri Mkuu, nafahamu mchakato wote ni kwamba kweli tulikuwa na mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii ambayo inashughulikia mafao ya watumishi waliostaafu. Tulikuwa na LAPF chini ya Ofisi ya Rais, wakati huo ilikuwa Waziri Mkuu, tukawa na mifuko mingi, lakini tukaipunguza mifuko hii tukaacha michache ili iweze kulipa vizuri maslahi kwa watumishi waliostaafu. Sasa tuna NSSF ambayo pia inashughulikia sekta binafsi na wachache sekta rasmi, na pia kuna PSSSF baada ya kuwa tumebadilisha sheria hiyo.

Mheshimiwa Spika, ulipaji wa mafao unaendelea siyo kwa kiasi kikubwa, ni kwa sababu mifuko hii ilipoanzishwa tulikuta madeni mengi na makubwa. Kazi ambayo inafanywa sasa ni kulipa madeni ya wastaafu wa muda mrefu na tunaendelea kulipa wale wanaostaafu ili angalau kukamilisha hili, tufike hatua ya kuweza kulipa madeni pindi mtumishi anapostaafu na kuendelea kulipwa mafao yao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mabadiliko ya sheria yapo na kanuni zilitengenezwa. Kwa sasa tunaangalia kama kanuni na sheria hizi zinaweza kutufikisha hatua nzuri ya kulipa mafao kwa wakati. Tayari Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Ajira na Vijana ndio anasimamia jambo hili; na wakati wote amekuwa na vikao na mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii ili kuhakikisha kwamba inalipa kulingana na wakati aliostaafu mtumishi; wale wa zamani na walioko sasa. Ulipaji unaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayo madai, lakini pia tunaendelea kupata changamoto za kutokamilisha ipasavyo kulipa wadai wote kwa sababu ya yale madeni. Serikali iliwahi kutoa fedha kwa ajili kuongezea uwezo wa mifuko yetu ili iweze kulipa mafao na kazi hiyo inaendelea. Kwa hiyo, tutaendelea kufanya mapitio ya sheria hizo na Waziri wa Nchi yuko hapa, anaendelea kusimamia. Malengo yetu ni kulipa watumishi wote wanaostaafu kwa wakati na hatua hii nina uhakika tutaifikia. Ahsante sana. (Makofi)