Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Aysharose Ndogholi Mattembe (32 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania ni nchi ya kilimo. Asilimia 80 ya wananchi wa Tanzania wanategemea kilimo. Ili kupunguza umasikini na kuondoa utegemezi wa nchi wahisani, ni lazima tuwekeze kwa kiasi kikubwa katika kilimo na tuwe na mikakati thabiti ya kukiboresha kilimo chetu. Hivyo basi, hatuna budi kilimo chetu sasa kijielekeze katika kuongeza uzalishaji kwa ekari moja na kuachana kabisa na ukulima wa jembe la mkono. Kwa mfano, nchi kama China wamefanikiwa sana katika kilimo cha uzalishaji kwa ekari moja. Ukilinganisha ukulima wao na wetu, wakulima wetu wanalima ekari tatu mpaka nne lakini wanapata mazao ya ekari moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida kijiografia ni mkoa wenye hali ya ukame ambao unapata mvua kwa msimu mmoja na unakabiliwa na changamoto nyingi katika Sekta ya Kilimo. Kwa hiyo, kuna haja ya Serikali kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Singida waweze kulima na kunufaika na kilimo cha matone kwenye maeneo yenye chemchemi na maeneo ambayo hayana chemchemi, basi Serikali iwasaidie kuchimba mabwawa ya maji ili waweze kulima na kuvuna kwa misimu yote ya mwaka. Maeneo ambayo yamenufaika na kilimo cha matone Mkoani Singida ni Isana, Mkiwa, Uhamaka na Kisasida.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida pia unakabiliwa na uhaba wa Maafisa Ugani pamoja na mashamba darasa. Naomba Serikali iunge mkono jitihada za uanzishwaji wa mashamba darasa kwani yana mchango mkubwa wa maendeleo ya kilimo, siyo tu kwa kuwafundisha wakulima kwa niaba ya Maafisa Ugani, bali pia husaidia kutoa utaalam wa kuzalisha mbegu bora za daraja linalokubaliwa, yaani QDS.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida ni mkoa unaosifika kwa kilimo cha alizeti, mahindi, mtama, uwele, karanga na vitunguu, lakini bado wakulima wake hawajanufaika na ukulima huo na hii ni kutokana na ukosefu wa soko la kudumu au vituo maalum vya kuuzia mazao yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali ya Awamu ya Tano kuona umuhimu wa kujenga soko kubwa la kisasa la mazao kwenye Manispaa ya Singida, kwani uwepo wake utatoa nafasi kwa wakulima wengi kunufaika na bei za mazao yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida unakabiliwa pia na ukosefu wa vituo vya utafiti ikiwemo maabara ya matumizi ya udongo na hii hupelekea wakulima wengi wasiweze kujua hali ya ardhi yao na hivyo kusababisha uzalishaji duni. Naomba Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kulitazama kwa kina na kuona ni namna gani wataweza kuwasaidia wakulima wetu katika kutambua matumizi bora ya ardhi ili kuongeza uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa mifugo, Singida ni hodari wa ufugaji wa ng‟ombe, mbuzi na kondoo lakini bado zipo changamoto kadhaa zinazokwamisha maendeleo ya mifugo Mkoani Singida. Changamoto hizo ni uhaba wa majosho, uhaba wa maeneo ya malisho na magonjwa ambayo kwa asilimia 70 yanachangiwa na mdudu kupe. Hivyo basi, naiomba Serikali yangu sikivu kuongeza majosho ya kutosha, kutenga maeneo ya malisho na maji na kuleta dawa za chanjo na dawa hizo zifike kwa wakati.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuunga hoja mkono. Tanzania ni nchi yenye rasilimali nyingi ambapo kama zitatumiwa vizuri katika viwanda vyetu zitaleta manufaa makubwa sana katika Tanzania yetu. Hata hivyo, changamoto kubwa inayovikabili viwanda nchini ni ukosefu wa mitaji, teknolojia, umeme, malighafi zisizokuwa za uhakika pamoja na ukosefu wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na changamoto niliozitaja hapo juu bado hakuna vivutio vizuri kwa wawekezaji kutoka nchi za nje na mlolongo wa kodi nyingi ambazo zinawavunja moyo wawekezaji wa ndani na nje. Ningeshauri Serikali kwa changamoto ambazo nimezitaja hapo hasa za ukosefu wa umeme, teknolojia na maji ni vema sasa Wizara ya Viwanda ikakaa pamoja na kuwa na mikakati ya pamoja na Wizara ya Nishati, Kilimo na Maji ili kuunganisha nguvu kwa pamoja na kuwa na mkakati mmoja kwa kuwa Wizara nilizozitaja hapo juu zina mahusiano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mlolongo wa kodi ni vema sasa Serikali ikawa na chombo kimoja ambacho kitakuwa na mamlaka ya kutoza kodi ambacho kitasimamia utozaji wa kodi zote kwa wawekezaji. Mkoa wa Singida ni mkoa unaosifika kwa uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara. Mazao ya biashara ni alizeti, vitunguu, pamba, ufuta, karanga na choroko. Mazao ya chakula ni mahindi, mtama, viazi vitamu na uwele, lakini bado hakuna viwanda vya kutosha. Pia Singida ni wafugaji wa ng’ombe, mbuzi na kondoo. Mazao yote niliyotaja hapo juu yangeweza kuwa malighafi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika viwanda mbalimbali ambavyo vingeanzishwa Mkoa wa Singida. Mkoa wa Singida ni maarufu kwa ukulima wa alizeti, alizeti inayozalishwa Singida ni maarufu Afrika Mashariki na Kati. Singida ina jumla ya viwanda 126 vya alizeti, kikubwa kimoja, vitatu vya kati na vidogo vidogo 122. Hivi vidogo vidogo vinategemea mitaji kutoka SIDO.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeishauri Serikali yangu kuona uwezekano wa kuwaongezea uwezo SIDO, ili waweze kuwakopesha viwanda vidogo vidogo mitaji ya kutosha. Kwa sasa SIDO inakopesha shilingi milioni sita. Iwapo itaongezewa uwezo angalu kuwakopesha wajasiriamali wa viwanda vidogo vodogo milioni ishirini itakuwa ni jambo jema sana. Kwani wajasiriamali wadogo wadogo hawana uwezo wa kwenda kukopa kwenye benki na taasisi mbalimbali za fedha kwa kuwa wanatoza riba kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningeomba Wizara hii kuuangalia Mkoa wa Singida kwa jicho la pekee kwa sababu kila Wilaya/Halmashauri tayari kuna maeneo kwa ajili ya kuanzisha viwanda, kinachokosekana ni mitaji, hivyo iwapo Serikali itapata mitaji itasaidia sana kuweka miundombinu ya viwanda kwa kuwa malighafi si za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Waziri wa Viwanda Mheshimiwa Mwaijage kwa kazi nzuri anayoifanya katika kuleta mageuzi katika viwanda yeye pamoja na timu yake, nawatia moyo waendelee kukaza buti kazi ni nzuri na yenye tija.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kutoa mchango wangu katika bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi.
Awali ya yote namshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, mwingi wa neema ambaye ameniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza sana Rais wetu mpendwa Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuliongoza Taifa hili.
Vilevile nampongeza Makamu wa Rais Mheshimiwa Mama Samia Suluhu, Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Baraza la Mawaziri kwa namna ambavyo wanajituma kuhakikisha kero za Watanzania zinapungua au zinakwisha kabisa. Ninapenda kuwatia moyo waendelee kukaza buti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii pia kuwashukuru sana wananchi wa Mkoa wa Singida hususan wanawake na vijana kwa kuniamini na kunichagua kwa kura nyingi za ndio napenda kuwahakikishia kwa heshima hii kubwa waliyonipa sitawaungusha na wala sitaanguka katika kuwatumikia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo najielekeza moja kwa moja katika kuchangia. Mwanafalsa mmoja John Dew aliwahi kusema education is not preparation for life, education is life itself, akimaanisha kuwa elimu siyo maandalizi ya maisha, elimu ni maisha yenyewe, hivyo basi, elimu ndiyo msingi mkuu katika kuyamudu maisha ya kila siku na ndiyo mkombozi wa maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania inatajwa kuwa na elimu ya kiwango cha chini ukilinganisha na nchi nyingine za Afrika Mashariki, hii ni kutokana na ukweli kwamba elimu inayotolewa haikidhi viwango vya ubora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu inayotolewa katika vyuo na shule zetu za Serikali haimuandai kijana kujiamini, kuwa mbunifu, kuwa ni mwenye uwezo wa kubembua mambo, kuwa na communication skills, kuweza kujiajiri au kuajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii kijana aliyemaliza elimu ya kidato cha nne kutoka nchini Kenya au Uganda akija Tanzania anapata ajira bila wasiwasi wowote, hii ni kwa sababu elimu aliyopata ni bora, inamwezesha kujiamini, inamwezesha kujielezea kwa ufasaha kwa lugha ya kiingereza ambayo hapa nchini kwetu ni lugha ya biashara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo sababu kadhaa ambazo zinachangia kushuka kwa kiwango cha elimu katika shule zetu za Serikali. Sababu hizi nitazitaja kama ifuatavyo:-
Kwanza, ni utayarishaji wa mitaala ambayo haiendani na wakati na mazingira ya sasa. Mitaala ambayo inakosa skills ambazo zingeweza kumsaidia mwanafunzi kujiamini au kujitegemea baada ya kumaliza elimu yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti zimeonyesha kwamba kuna changamoto za utayarishaji na utekelezaji wa mitaala bila kufanyiwa majaribio jambo linalopelekea walimu wengi kukosa stadi za maisha, kukosa maarifa ya kufundishia. Mfano katika Taifa la Netherland mtaala wake unasisitiza kufundisha elimu ya ujasiriamali kuanzia shule za sekondari. Hivyo basi, ningeishauri Serikali kutizama upya mitaala ambayo itazingatia uchambuzi wa kina wa kumwezesha kijana kuweza kujitegemea na kujiamini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya pili inayochangia kushuka kwa kiwango cha elimu, ni uhaba wa vitendea kazi na teaching methodology ambazo kimsingi hazimjengi mwanafunzi kujitegemea au kujiamini. Shule zetu nyingi za Serikali zinafundisha kwa nadharia zaidi kuliko vitendo. Wenzetu wa dunia ya kwanza wanasema practice makes perfect. Unapomfundisha mwanafunzi kwa nadharia na vitendo unamwezesha mwanafunzi huyo kulielewa somo hilo vizuri zaidi. Hivyo kuna haja ya msingi ya kurudisha elimu ya vitendo katika shule zetu za msingi na sekondari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, ukimfundisha mwanafunzi mapishi ya keki kwa nadhari na baadaye ukaweza kumuonyesha namna ya keki hiyo inavyopikwa ataelewa zaidi. Kusoma kwa nadharia tu ni sawa na kuwa-feed wanafunzi kitu ambacho hawana reference nacho. Hivyo basi, ningeomba sana elimu ya vitendo ilirudishwe kama zamani ilivyokuwa ikifundishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo linachangia elimu yetu kuendelea kuwa duni ni kukosekana kwa uwiano kati ya mwalimu na wanafunzi darasani katika shule zetu wanafunzi katika darasa moja wanaweza kufikia idadi ya wanafunzi 35 mpaka 50, idadi hii inamuwia mwalimu ugumu kuweza kufanya assessment kwa kila mwanafunzi. Matokeo yake anaangalia tatizo la mwanafunzi mmoja na kulitolea suluhu kwa wanafunzi wote darasani. Tofauti ya darasa lenye wanafunzi kumi mpaka kumi tano, ni rahisi mwalimu assessment ya kila mwanafunzi na kujua wana tatizo gani pindi atakapomaliza kufundisha na kuona namna gani ya kuwasaidia hao wanafunzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutomuandaa mwalimu vema ili afundishe kuendana na wakati wa sasa nayo ni sababu inayochangia kuporomoka kwa elimu yetu. Ajira ya ualimu imewekwa katika kundi la kitu ambacho hakina thamani. Leo hii wanaochukuliwa kujiunga na ajira hii ni wahitimu waliopata daraja la nne katika kidato cha nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine maslahi ya walimu ni duni. Mwalimu kwa kweli hawamjali mwalimu, mwalimu huyu hana nyumba ya kuishi, anaishi katika mazingira duni, mshahara wake ni mdogo na wala haumkidhi mahitaji yake na wakati mwingine haufiki kwa wakati. Ningeiomba Serikali yangu kuwaangalia walimu na kuangalia maslahi yao upya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unategemea nini kwa mwalimu kama huyo na atakuwa kweli na morali ya kufundisha si ata-beep tu kutimiza wajibu wake na kuondoka zake. Ndiyo maana kiwango cha elimu kimeendelea kushuka kutoka asilimia 22.3 mwaka 1985 na kufikia asilimia 49.6 mwaka 2010.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishauri Serikali kuja na mpango utakaowawezesha walimu kupata training za mara kwa mara na semina zinazolenga mahitaji ya sasa ili kuwawezesha kufundisha kwa ufanisi na ufasaha katika dhama hizi za sayansi na teknolojia. Lakini pia vilevile walimu watakaokuwa wamejiendeleza wapewe incentives kulingana na madaraja yao, hii itasaidia sana kupunguza madai ya uhamisho ya mara kwa mara na kuwafanya walimu watulie katika maeneo yao ya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiofichika kwamba katika shule zetu za Serikali hatuna programu za kuhamasisha watoto wapende kusoma vitabu, wanafunzi wetu hawana tabia ya kujisomea vitabu, lakini pia vitabu vyenyewe hakuna vya kutosha. Serikali ione umuhimu wa kuanzisha programu au iwena slogan maalum ambayo itawahamasisha wanafunzi wetu na katika kila mkoa uwe na e-library ambayo wanafunzi watapata ku-access vitabu mbalimbali zikiwemo story books ambazo zitaweza kuwasaidia katika ku-improve english language ambayo ni medium of instruction in secondary schools.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Singida ni miongoni mwa mikoa yenye changamoto nyingi katika sekta ya elimu. Mkoa wa Singida una jumla ya shule 542, kwa wastani kwa mwaka watoto 25,000 humaliza shule ya msingi ukilinganisha na ufaulisha watoto 13,383 kwa mkoa mzima. Ukilinganisha idadi hii ya wananfunzi waliomaliza shule za msingi hailingani kabisa na wale wanaondelea na masomo ya shule za sekondari. Zaidi ya vijana 10,000 wanakaa mitaani…
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia mjadala ulioko mbele yako sasa. Awali ya yote namshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, mwingi wa neema kwa kunijalia uzima na afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kutoa pole kwa Watanzania wote, familia, ndugu, jamaa na marafiki kwa msiba uliotufika wa kuondokewa na Spika Mstaafu, Marehemu Mzee Samuel Sitta. Enzi za uhai wake aliweza kutoa mchango mkubwa wa maendeleo katika Taifa hili hivyo basi hatuna budi kumuunga mkono na kumuenzi kwa vitendo vyake vizuri. Tunamuomba Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi, Amina. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na umuhimu wa Halmashauri katika kuleta maendeleo ya Taifa hili bado kuna ubadhirifu mkubwa wa watendaji wa Halmashauri katika usimamizi na utekelezaji wa miradi na hii husababisha miradi kutokukamilika kwa wakati na mingine kuvunjika kinyume cha mikataba. Ukitazama kitabu hiki cha taarifa yetu, ukurasa wa 8 utaweza kuona baadhi ya mifano ya miradi ambayo haijakamilika au kutekelezeka. Mfano, mradi wa maji katika Kijiji cha Kayenze Jijini Mwanza wenye thamani ya shilingi milioni 618.7, mradi huu haukutekelezwa. Mradi wa maendeleo wa shule ya sekondari wa ujenzi wa bweni wenye thamani ya shilingi milioni 94.2 katika Kijiji cha Ndogosi na shilingi milioni 100.13 katika Kijiji cha Ruanda katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ambao haujakamilika na mifano mingine inajionesha hapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe katika Kamati ya LAAC. Katika utekelezaji wa majukumu yetu, tumebaini mambo mengi hayako sawa katika Halmashauri zetu kwani kuna ubadhirifu mkubwa wa rasilimali za umma pamoja na matumizi mabaya ya fedha ambayo yanakinzana na sheria na kanuni za fedha za Serikali za Mitaa. Hapa naishauri Serikali kuweka sheria kali na kuzisimamia kwa uwazi ili watendaji ambao wanakwenda kinyume na matarajio ya Watanzania na kinyume na dhamira safi ya Mheshimiwa Rais wetu ambaye anataka kuona nidhamu katika rasilimali za umma washughulikiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mara kwa mara tunakaa hapa tukiwajadili watendaji wabadhirifu wa mali za umma wakati sheria zipo kwani hawa watendaji wana pembe? Kwa nini wasishughulikiwe kikamilifu? Nini commitment ya Serikali juu ya jambo hili? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakati mwingine Serikali inahusika kwenye udhaifu huu kwa kuwaacha watendaji wa Halmashauri kwenye kituo kimoja kwa muda mrefu. Hii humfanya mtendaji kujisahau au kufanya kazi kwa mazoea na wakati mwingine watendaji wengine kukaimu nafasi zao kwa muda mrefu. Kama wana uwezo kwa nini wasithibitishwe? Kama hawana uwezo kwa nini wasiondolewe katika nafasi hizo ili tuweze kuwabana vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumebaini Halmashauri nyingi hazizingatii Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2011, aidha, kwa makusudi au kwa matakwa yao binafsi. Tulibaini baadhi ya Halmashauri zinafanya manunuzi ya bidhaa na huduma nje ya bajeti husika wakati kanuni zinazitaka kufanya manunuzi kulingana na bajeti zilizoidhinishwa. Katika Halmashauri nyingine hakukuwa na kamati za manunuzi hivyo kutokudhibiti ubora na idadi ya bidhaa kulingana na thamani ya pesa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tulibaini baadhi ya watendaji hutoa zabuni kwa wazabuni ambao hawana sifa wala vigezo vya kupewa zabuni hizo na kusababisha mikataba mingi kuvunjika kabla ya utekelezaji wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali iendelee kuwabana watendaji ambao hawazingatii kikamilifu Sheria ya Manunuzi ya Umma ambao mara nyingi wamekuwa wakiitia hasara Serikali na kusababisha upotevu wa fedha za umma. Kwa upande mwingine naiomba Serikali kupeleka pesa za miradi ya maendeleo kwa wakati kwani kwa kufanya hivyo wataweza kuondoa mianya ya kupanda gharama za miradi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na changamoto nilizozitaja hapa juu naongea kwa masikitiko makubwa juu ya jambo hili, Halmashauri zetu nyingi zimekuwa hazipeleki 10% kwenye Mfuko wa Wanawake na Vijana na hii imesababisha vijana kutokupata fursa za kujiajiri au kufanya miradi ya maendeleo. Fedha hizi zingekuwa zinapelekwa kwa wakati zingeweza kusaidia vijana kujiajiri au kujikwamua kiuchumi. Mbali na watendaji kushindwa kupeleka 10% kwa vijana na wanawake lakini pia wameshindwa kupeleka 20% za fedha zinazotoka Serikali Kuu kwa vijiji kana kwamba pesa hizo ni za hisani na siyo lazima. Kwa hiyo, naiomba Serikali, kwa kuwa hakuna sheria za kuwabana watendaji kupeleka kwa wakati 10% kwa vijana na wanawake na 20% kwa vijiji itunge sheria ili kuhakikisha agizo hili linatekelezwa kwa wakati na kwa mtiririko unaofaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamezungumzia mengi, kwa haya machache naomba niishie hapa. Ahsante kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyo mbele yetu. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na neema kwa kutujalia uzima na afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza sana Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Simbachawene, lakini pia na Naibu wake Mheshimiwa Jafo pamoja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Angellah
Kairuki. Napenda kuwapa moyo mnafanya kazi nzuri, endeleeni na moyo huo huo na kazeni buti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo moja kwa moja nijielekeze kwenye hoja iliyopo mezani nikianza na suala la elimu bure. Napenda kuipongeza Serikali kwa mafanikio makubwa waliyoyapata kwa muda mfupi kwa kutoa elimu bure. Jambo hili limejidhihirisha wazi, kwa mwaka 2017 jumla ya wanafunzi milioni 3.8 wa darasa la awali na la kwanza waliweza kuandikishwa. Uandikishaji huo ni sawa na
ongezeko la wanafunzi 300,000 ambao waliweza kuandikishwa kwa mwaka 2016. Ongezeko hilo limechangiwa na wazazi wengi kuhamasika na Waraka wa Elimu Bure na kupeleka watoto wao shule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini elimu bure imekuja na changomoto zake zikiwepo uhaba wa madawati, vyumba vya walimu, vyumba vya madarasa, upungufu wa walimu na matundu ya vyoo. Mfano kwa Mkoa wa Singida kuna upungufu wa madarasa 5,547 na nyumba za walimu 5,580. Idadi hii ni kubwa sana ambapo kwa bajeti zilizotengwa katika Halmashauri zetu haziwezi kukamilisha ujenzi wa miundombinu kwa kukarabati shule zetu zilizoko vijijni na hata zilezilizojengwa chini ya mpango wa MMEM I na MMEM II. Hali ni mbaya na hasa kwa shule zetu zilizopo vijijini ambazo hazimfanyi mwalimu kufundisha kwa utulivu, lakini vile vile hazimfanyi mwanafunzi kupokea kile anachofundishwa na
mwalimu. Bila mazingira bora ya kufundishia hakuna elimu bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kwa Wilaya ya Ikungi tu pekee, ina uhaba wa shule 568 na upungufu wa walimu 490, vilevile ina uhaba wa vyumba vya madarasa 568. Hivyo, naiomba Serikali yangu sikivu kuangalia mpango mahususi ambao utawezesha ujenzi wa miundombinu hii ya elimu kukamilika, lakini pia kuboresha mazingira ya kufundishia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuweza kujenga maabara 5,562, lakini ni ukweli usiopingika, miundombinu ya maabara zetu bado hazijakaa vizuri na hasa maabara zilizopo katika Mkoa wangu wa Singida.
Naishauri Serikali kukamilisha miundombinu hiyo kwa haraka iwezekanavyo ili kuwawezesha wanafunzi hao kujifunza masomo ya sayansi kwa vitendo, lakini pia kwa ukamilifu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda, bila ya kuwandaa wanafunzi wetu kuwa wanasayansi, ni vipi tutayafikia malengo yetu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninalotaka kuchangia ni suala la watumishi wa umma. Wapo madaktari na wauguzi ambao wanatazama afya za Watanzania, lakini pia wapo walimu ambao pia ndiyo msingi wa maendeleo kwa kwa Taifa letu. Bila elimu bora hakuna maendeleo na bila walimu bora hakuna mambo yatakayoweza kufanyika kwa weledi, ujuzi na ufanisi. Watumishi hawa wamekuwa
wakifanya kazi kubwa na ngumu na bado maslahi na stahiki zao zimekuwa ni ndogo sana ukilinganisha na kazi wanazozifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuchangia na ninaona siyo zuri pia kwa watumishi, ni watumishi wengi kutokupandishwa madaraja kwa wakati. Jambo hili linawavunja sana moyo watumishi wa umma. Ninatambua kwamba zoezi la uhakiki wa watumishi wa umma limekamilika, hivyo basi ni wakati muafaka wa kuwapa watumishi wetu kile kinachostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la afya. Sera ya Afya ya mwaka 2007 imehitaji kila kijiji kuwa na zahanati moja, lakini katika Wilaya ya Singida ambayo ina kata 21 kuna zahanati 26 tu ambazo hazikidhi mahitaji ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile zahanati zilizopo zina upungufu mkubwa wa vifaa tiba lakini pia na wataalamu. Jambo hili linasababisha msongamano sana katika hospitali zetu za Wilaya, lakini pia vilevile msongamano katika hospitali yetu ya rufaa ya Mkoa wa Singida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali inakuwa ni mbaya zaidi pale mama mjamzito anapohitaji huduma ya afya katika zahanati zetu ambapo hakuna huduma za upasuaji, hakuna theatre, hakuna huduma za damu safi na salama. Unategemea mama mjamzito aende wapi iwapo atakumbwa na kadhia hii ya kwenda kujifungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuchangia ucheleweshaji wa fedha za miradi ya maendeleo. Nakubaliana na mfumo wa Serikali kwamba baadhi ya mapato kuingizwa moja kwa moja kwenye mfuko wa Serikali Kuu na naipongeza sana Serikali, lakini mfumo
huu una changamoto zake. Moja ya changamoto ni kusababisha baadhi ya Halmashauri kutokutekeleza majukumu yake kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua hapo awali kabla ya kutumika kwa mfumo huu kulikuwa na mianya mingi ya rushwa na upotezaji wa fedha za umma, lakini kwa sasa hali ya fedha za miradi ya maendeleo zitoke kwa wakati ili kusaidia kuharakisha upatikanaji wa huduma kwa jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni kuhusu Madiwani wetu. Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia wamechangia kuhusu Madiwani. Madiwani wanafanya kazi ngumu; wa ndio kiungo kati ya Wabunge na wananchi. Tunapokuwa huku Bungeni kufanya shughuli
zetu, wenyewe wanakuwa karibu na wananchi. Hivyo, naomba Serikali iangalie Madiwani wetu na Wenyeviti wa Vijiji kwa jicho pana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Singida ni miongoni mwa mikoa inayokabiliwa na changamoto nyingi za afya kuanzia vijijini hadi manispaa. Kwa sasa kuna vituo vya afya 17 tu wakati tunatakiwa kuwa na vituo vya afya 117 ili kuhudumia wananchi wa kata 134 za Mkoa wote wa Singida. Sera ya Afya ya mwaka 2007 inatuelekeza kuwa na kituo cha afya kwa kila kata na zahanati kwa kila kijiji, hivyo hilo ni tatizo kubwa katika utoaji wa huduma za afya kwa wananchi waishio vijijini ambako kuna changamoto nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua katika kukabiliana na hali hii kuna vituo vya huduma za afya 69 ambavyo ujenzi wake uko kwenye hatua mbalimbali. Ninaomba Serikali iongeze nguvu kuhakikisha vinakamilika haraka ili tuokoe afya za wananchi wetu na kuendelea kujenga Taifa lenye watu wenye afya njema. Lakini nisisitize kwa Serikali kwamba ujenzi wa vituo hivyo uendane sambamba na uboreshaji wa usambazaji wa vifaa tiba pamoja na dawa muhimu kulingana na mahitaji, miundombinu, watumishi na maslahi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tatizo kubwa la uhaba wa watumishi kwenye mkoa wangu wakiwemo Madaktari Bingwa hasa wale wa magonjwa ya akina mama ambapo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa peke yake inatakiwa kuwa na Madaktari Bingwa 32 lakini waliopo ni watano tu kwa mkoa mzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Singida una upungufu wa watumishi wa afya wa kada mbalimbali 305. Hii ni idadi kubwa sana wakati vyuo vyetu vinazalisha wataalam kila mwaka. Ni kwa nini hawa wataalam tusiwasambaze kwenye vituo vyetu vyenye ukosefu wa wataalam?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuiomba sana Serikali yangu kuendelea kusimamia kwa haki na kuendelea kuboresha maslahi ya watumishi wa kada ya afya ambao ni watu muhimu sana na wanafanya kazi kubwa sana na kwenye mazingira magumu. Watumishi wa afya wote wanaostahili kupandishwa madaraja na nyongeza za mishahara wapewe stahiki hizo kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwenye mkoa wangu kuna watumishi ambao hawajapandishwa madaraja kwa muda mrefu ikiwemo sababu ya Serikali kufanya uhakiki. Zoezi hilo limekwisha hivyo Serikali itimize wajibu wake. Zoezi hilo la kupandisha madaraja na maboresho ya mishahara yaende sambamba na mazingira bora ya kufanyia kazi kwa watumishi wa afya ambao wengi wao wa vijijini hawana makazi bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi hayana nyumba za watumishi, ofisi hazina hadhi, hivyo nina imani kubwa Mheshimiwa Ummy atauangalia Mkoa wa Singida ambao unapokea na kuhudumia wagonjwa wengi wakiwemo wanaopatwa na majanga kama ajali. Mkoa wetu unahitaji nyumba bora 1,072 lakini zilizopo ni 345 kwa mkoa mzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naiomba Serikali kuangalia kwa umakini afya za wanawake na kutoa kipaumbele katika kupambana na ugonjwa hatari wa saratani ya kizazi na matiti ambao umekuwa tishio kubwa. Nashauri vianzishwe vitengo vya saratani kwenye Hospitali zote za Rufaa za Mkoa badala ya wagonjwa kujazana pale Taasisi ya Ocean Road ambayo ni ukweli kuwa imezidiwa sana. Umefika wakati sasa kuanza mikakati kabambe ya kudhibiti ugonjwa huo kuanzia ngazi za vijiji kwa kufanya upimaji na kampeni za uchunguzi wa mara kwa mara hasa maeneo ya vijijini ambako wagonjwa wengi hufika hospitalini wakati ugonjwa ukiwa umekithiri sehemu kubwa ya mwili wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nazindua kampeni yangu ya Kijana jitambue, wakati ni sasa ambayo ilitoa stadi za maisha kwa vijana kujitambua utu wao na mbinu za kujikwamua kiuchumi, tuliendesha pia zoezi la upimaji saratani ambapo wanawake wengi walipata fursa hiyo na wengine kubainika kuwa na tatizo hilo na kuelekezwa namna ya kupata huduma. Kwa hiyo, jambo hilo limejidhihirisha wazi kuwa wanawake wengi waliopo vijijini wameathirika na saratani ya shingo ya kizazi na matiti lakini wanakuwa hawajitambui kama wameathirika kutokana na kukosa huduma za awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya ya Mtanzania ndicho kitu muhimu cha kwanza kabisa kwani kama hatutakuwa na afya njema basi maendeleo ya nchi yetu yatazorota na kuwa nyuma, hivyo, Serikali inapaswa kuendelea kutoa kipaumbele kikubwa katika mapato yake katika Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, ili kupunguza vifo vya akina mama na watoto ifike wakati sasa zahanati zetu na vituo vya afya viwe na wataalam wa kutosha, vifaa tiba vya kutosha na dawa za kutosha. Iwapo tutaimarisha huduma katika vituo vya afya na zahanati zilizopo zitasaidia sana kupunguza vifo vya akina mama na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia Wizara hii muhimu kwa mustakabali wa maisha ya wananchi wangu wa Mkoa wa Singida na Watanzania kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye amenijaalia afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Naipongeza sana Serikali ya CCM na Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri na kubwa wanayoifanya ya kuwaletea Watanzania maendeleo ya haraka na yenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mfupi Serikali ya Awamu ya Tano imeweza kufanya mambo mengi na makubwa. Mfano, ujenzi wa reli ya kisasa, uboreshaji wa miundombinu ya barabara na madaraja, utoaji wa huduma bora za afya na elimu na kujenga nidhamu katika rasilimali za Taifa letu. Hii yote inaonesha jinsi gani Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli alivyo makini na timu yake. Nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunatambua kwamba maji ni uhai katika maisha ya mwanadamu. Maeneo ambayo hayana maji hakuna maendeleo, shughuli nyingi za kiuchumi na kijamii zinategemea uwepo wa maji, hivyo basi ningeishauri Serikali kuangalia uwezekano wa kutunisha Mfuko wa Maji kwa kuongeza tozo ya maji ya lita ya petrol na diesel kutoka shilingi 50 hadi shilingi 100 ili kutunisha Mfuko huo kwani mfuko huo wa maji umekuwa ni mkombozi mkubwa kwa maendeleo ya miradi mingi ya maji katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanufaika wengi wa Mfuko huu wa Maji ni wale wanaoishi mijini. Hata ukitazama katika kitabu cha bajeti ya maji ukurasa 192 hadi 193 unaweza ukaona kwamba miradi mingi iliyonufaika ni ile iliyoko mijini hivyo ningeiomba Serikali kuangalia uwezekano wa kupeleka angalau asilimia 70 ya makusanyo ya tozo hii iende maeneo ya Vijijini ambako ndiyo kwenye matatizo makubwa ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuweza kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025 na kufanikisha malengo ya uchumi wa viwanda ni vema sasa Serikali ikaangalia uwezekano wa maeneo mengi kupata maji kwa urahisi. Vilevile kuunda chombo cha usimamizi wa miradi ya maji vijijini kama ilivyo REA ili kupambana na changamoto za maji vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake wa Mkoa wa Singida ambao ni wachapakazi na wabunifu, kama maji yanapatikana wakati wote wanaweza kutumia fursa hii kwa kulima mazao ya chakula na biashara kwa mwaka mzima na kuongeza pato la Taifa. Lakini kwa Mkoa wa Singida mambo yamekuwa ndivyo sivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na adha kubwa wanayopata wananchi wa Mkoa wa Singida kutokana na ukosefu wa maji safi na salama, na changamoto nyingi zilizopo katika Mkoa wa Singida bodo bajeti ya mwaka huu ya miradi ya maendeleo ya maji imepunguzwa kutoka shilingi bilioni 6.7 kwa mwaka huu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kipekee nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia uzima na afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Naunga mkono hoja na nimpongeze sana Mheshimiwa Ndalichako na Naibu wake Mheshimiwa Injinia Manyanya pamoja na timu nzima kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuleta mageuzi katika sekta ya elimu. Bila elimu bora hakuna Taifa bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunatambua elimu ndiyo uti wa mgongo kwa Taifa lolote lile. Nikimnukuu Marehemu Nelson Mandela aliwahi kusema; “Education is the most powerful weapon you can use to change the world” akimaanisha elimu ndiyo silaha kubwa inayoweza kuibadilisha dunia. Kama kweli tunataka kuibadilisha dunia ya Tanzania ni vema sasa tukawekeza zaidi katika elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na mimba za utotoni. Suala hili limekwamisha jitihada za watoto wa kike kufikia malengo yao. Mkoa wa Singida ni miongoni mwa mikoa inayoongoza kwa mimba za utotoni. Kwa mwaka 2015 kulikuwa na mimba za utotoni 11,513 ambazo zilikuwa chini ya umri wa miaka 20. Miongoni mwa waliobeba mimba hizi walikuwa ni wanafunzi walioacha shule na wale walioolewa, idadi hii ni kubwa sana na inasikitisha, ni lazima tutafute suluhu ya jambo hili ili wanafunzi wa kike waweze kusoma vizuri na kuweza kufikia ndoto zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri Serikali kuja na mkakati au programu au kampeni katika shule zetu ambayo itamsaidia mtoto wa kike kuweza kujitambua, kujiamini, kujithamini utu wake, kuwa na vision na kuweza kufikia malengo. Tunataka mtoto wa kike wa Tanzania hii aweze kujitambua, aweze kujua anataka kwenda wapi na atafikaje huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukajenga hostel nyingi zenye uzio mrefu, lakini bila ya kumtengeneza mtoto wa kike, kumjenga kisaikolojia, kumpa elimu ya kutosha kuweza kujitambua itakuwa ni kazi bure na mimba za utotoni zitaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Serikali iliendesha zoezi la uhakiki wa vyeti vya taaluma kwa watumishi wa umma. Naipongeza Serikali kwa hatua hii kwani itasaidia kupata watumishi wenye sifa zinazostahili, lakini miongoni mwa watumishi waliokumbwa na kadhia hii ni walimu. Ningependa kufahamu ni walimu wangapi wa shule za msingi na sekondari walioathirika na zoezi hili la uhakiki wa vyeti na je, Serikali imechukua hatua gani za kuweza kuziba nafasi zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu ukiangalia shule nyingi nchini zikiwemo za Mkoa wa Singida zina uhaba mkubwa wa watumishi walimu. Kwa Wilaya ya Ikungi tu kuna upungufu wa walimu 348 hao ni walimu wa sayansi na sanaa na kwa Wilaya ya Singida Vijijini katika shule za msingi kuna uhaba wa walimu 754, idadi hii ni kubwa sana ukijumlisha na wale waliotumbuliwa katika zoezi la uhakiki wa vyeti hali hii inakuwa siyo nzuri. Naiomba Serikali yangu iangalie jambo hili kwa ukaribu na ipeleke walimu wa kutosha hasa katika Mkoa wa Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwalimu ndiye mdau mkubwa katika elimu, tukiweza kumtengeneza kisaikolojia na kimaslahi tunaweza tukamuwezesha mwalimu huyu kufikia malengo yake. Kila siku hapa tutakuwa tunaimba elimu yetu imeshuka viwango, ifike wakati sasa walimu wapewe stahiki zao, walimu wawezeshwe kuwa na mazingira bora ya kufundishia kwa maana ya kuwa na nyumba bora za makazi, maslahi bora, miundombinu bora ya kufundishia hapo tutakuwa tumemwezesha mwalimu kuweza kumfundisha mtoto wa Kitanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni maabara, Watanzania walio wengi wamejitolea kwa hali na mali kuhakikisha shule zetu zinapata maabara, maabara nyingi hazina vifaa na hazina miundombinu inayoridhisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishukuru sana Serikali yangu kwa kusambaza vifaa vya maabara mashuleni lakini nielezee masikitiko yangu katika Mkoa wa Singida ni shule 18 tu ndiyo zilizopata mgao wa vifaa vya maabara. Idadi hii ni ndogo sana ukilinganisha na mikoa mingine na kama tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda tutafikaje huko bila ya kuwa na wataalam wa kutosha ambao watakuwa wameandaliwa vizuri katika maabara zetu? Nakuomba sana Mheshimiwa Ndalichako najua wewe ni msikivu, uuangalie kwa kipekee Mkoa wa Singida kwa kupeleka vifaa vya maabara vya kutosha pia vitabu vya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni Idara ya Ukaguzi. Serikali imekuwa ikitumia rasilimali nyingi kuboresha elimu hasa katika shule za sekondari. Nadhani ifike wakati sasa tuwekeze nguvu kubwa katika idara zetu za ukaguzi vinginevyo tutakuwa tunatwanga maji kwenye kinu. Ni lazima ukaguzi wa shule za msingi, sekondari na vyuo vikuu upewe msukumo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii muhimu iliyopo mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia uzima na afya njema na hatimaye kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Nampongeza Rais wangu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri wote kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuliongoza Taifa hili na kuhakikisha maendeleo ya haraka na yenye tija yanapatikana kwa Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha mapinduzi kwenye uchumi wa viwanda yanapatikana na hii itafanikiwa tu iwapo tutakuwa na mikakati thabiti ya kilimo chenye tija. Asilimia 80 ya wakazi wa Mkoa wa Singida wanajishughulisha na kilimo, hulima mazao ya mahindi, uwele, mtama, viazi vitamu na muhogo kama mazao ya chakula. Pia hulima mazao ya biashara kama alizeti, vitunguu, pamba, karanga pamoja na choroko lakini wanakabiliwa na changamoto nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hizo ni pamoja na pembejeo zisizokuwa na viwango, bei kubwa za pembejeo za zana za kilimo, ruzuku ndogo inayotolewa na Serikali, uhaba wa wataalam na mashamba darasa pamoja na uhaba wa mitaji na mikopo kwa wakulima. Hii inawakatisha tamaa sana vijana na wanawake ambao wengi wana hamasa kubwa ya kujikita katika kilimo cha kisasa lakini hukimbilia mijini ambapo hudhani ndiko kuna maisha bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mkoa wa Singida unakabiliwa na uhaba mkubwa sana wa Maafisa Ugani ambao ni watu muhimu sana katika kilimo na hasa kwa wale wananchi waliopo maeneo ya vijijini. Ukiangalia tu Wilaya ya Iramba, wapo Maafisa Ugani 79 lakini mahitaji ni 324, Wilaya ya Singida Vijijini mahitaji ya Maafisa Ugani ni 188 lakini waliopo ni 45 tu, Wilaya ya Mkalama mahitaji ni 185 lakini waliopo ni 38. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya uwepo wa Maafisa Ugani hao wachache, bado wanakabiliwa na ukosefu wa vitendea kazi kama pikipiki na hivyo kushindwa kuwafikia wananchi waliopo maeneo ya vijijini. Ni vema sasa Serikali ikaangalia jambo hili kwa kina kwa kuongeza Maafisa Ugani wa kutosha katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nielezee masikitiko yangu juu ya mgao mdogo wa ruzuku ya pembejeo kwa Mkoa wa Singida. Kwa msimu wa mwaka uliopita, 2016/2017, Serikali iliweza kutupatia tani 20 tu za mbegu za mpunga, tani 20 za mbegu za mahindi na tani 100 ya mbolea ya kukuzia ambayo ni sawa na asilimia 0.29 ya mbolea kwa mahitaji ya mkoa mzima. Kiwango hiki ni kidogo sana, mahitaji yetu ni kuanzia tani 33,000 mpaka 44,000 kwa mkoa mzima. Singida tumekuwa tukiachwa nyuma kwa kila jambo. Wakati ufike sasa wauangalie Mkoa wa Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Singida ni miongoni mwa mikoa inayolima mazao ya mafuta. Kwa Mkoa wa Pwani ni nazi, kwa Mkoa wa Kigoma ni mawese na Mikoa ya Singida na Dodoma ni alizeti. Hata hivyo, Serikali haijalitilia mkazo zao hili na haijalitaja kama ni zao la kimkakati, hata Mpango wa ASPD II haujatilia mkazo kabisa zao hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msimu uliopita takribani tani 58,000 ziliuzwa nchini Kongo ambazo ziliingiza zaidi ya shilingi bilioni sita. Iwapo zao hili litatiliwa mkazo uzalishaji utaweza kuongezeka lakini pia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana kwa mchango wako.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze sana Serikali kwa kazi nzuri inayofanya ya kuboresha huduma za afya nchini kote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuelezea changamoto za Hospitali yangu ya Rufaa ya Mkoa wa Singida. Hospitali hii inatoa huduma katika maeneo mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo hospitali ya rufaa ya zamani katika Kata ya Ipembe na hospitali mpya ya rufaa iliyopo katika Kata ya Mandewa. Uendeshaji wa hospitali hizi mbili kwa wakati mmoja imepelekea gharama za uendeshaji kuwa kubwa kwa kuwa inatumika bajeti moja kulipia bili ya maji, umeme, ulinzi na usafi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa nini sasa Serikali isimalizie Hospitali ya Rufaa ya Mandewa yale majengo muhimu kama maabara, pharmacy, wodi ya upasuaji kwa magonjwa ya kwaida na mifupa, wodi ya watoto, jengo la macho na jengo la meno? Iwapo majengo haya yatakamilika yatasaidia sana hospitali ya rufaa ya zamani iliyopo Kata ya Ipembe kuhamia hospitali ya rufaa mpya ya Mandewa. Naiomba Serikali itenge fedha za kutosha ili kumaliza Hospitali hii ya Rufaa ya Mandewa kwa kuwa majengo ambayo yalishakamilika yameanza kuchakaa hata kabla ya kutumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hospitali yangu ya rufaa ina changamoto lukuki; haina madaktari bingwa wa kutosha, waliopo ni sita tu na kati ya hao sita hakuna daktari bingwa wa magonjwa ya wanawake na watoto lakini pia ina wauguzi wachache. Wauguzi waliopo katika hospitali hii ni 144 kati ya 305 wanaotakiwa. Naomba Serikali itupatie watumishi wa kutosha wakiwemo wauguzi kwani hospitali hii ndiyo tegemeo la wananchi wa Mkoa wa Singida katika kupata huduma za afya za kibingwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hospitali hii pia haina gari la kubebea wagonjwa (ambulance), gari lililopo lilipata accident takribani miaka mitano iliyopita. Jambo hili nimekuwa nikilileta kwenu mara kwa mara, naomba sana sana kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Sindida ifike wakati sasa Hospitali hii ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ipatiwe gari la kubebea wagonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hospitali zangu zote za Wilaya ikiwemo ya Wilaya ya Iramba na Manyoni hazina magari ya kubebea wagonjwa. Naomba sana hospitali hizi za Wilaya zipatiwe magari ya kubebea wagonjwa ili kuokoa vifo vya akina mama na watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja. Dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha mapinduzi makubwa kwenye uchumi wa viwanda yanapatikana lakini tutafanikiwa tu iwapo tutakuwa na mikakati thabiti ya kulima kilimo cha kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali bado kuna changamoto nyingi ambazo hazina budi kupatiwa ufumbuzi wa haraka ili kuyafikia malengo ya uchumi wa viwanda. Tukilima kilimo cha kisasa tutapata malighafi za kutosha, tutapata chakula cha kutosha na kuweza kuuza mazao ya biashara ndani na nje ya nchi na tatizo la njaa nchini litageuka kuwa historia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 80 ya wakazi wa Mkoa wa Singida wanajishughulisha na kilimo na ndiyo ajira kubwa kwa vijana na wanawake. Hulima mahindi, mtama, mihogo, uwele, viazi vitamu kama mazao ya chakula na mazao ya biashara ni alizeti, vitunguu, pamba, ufuta na choroko lakini wanakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo:-

(i) Pembejeo zisizokuwa na viwango;

(ii) Bei kubwa ya pembejeo na zana za kilimo;

(iii) Uhaba wa wataalam na mashamba darasa ambayo husababisha uzalishaji kuwa mdogo;

(iv) Ukosefu wa mitaji na mikopo kwa wakulima;

(v) Ruzuku ndogo ya pembejeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hizi zilizotajwa hapo juu zinakatisha tamaa vijana na wanawake wengi ambao wana hamasa kubwa ya kujikita katika kilimo cha kisasa lakini wanashindwa kufanya hivyo na kukimbilia mijini wakidhani huko ndiko kwenye maisha bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maafisa Ugani ndiyo watu muhimu wa kuwapa mbinu bora za kilimo na hasa wakulima waliopo vijijini lakini Mkoa wa Singida una uhaba mkubwa wa maafisa hawa. Kwa Wilaya ya Iramba wako 79 wakati mahitaji ni 324; Wilaya ya Singida Vijijini mahitaji ni 188 lakini waliopo ni 45; Wilaya ya Mkalama mahitaji ni 185 na waliopo ni 38 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya uwepo wa Maafisa hawa wachache lakini nao wanakabiliwa na ukosefu wa vitendea kazi kama vile pikipiki na hivyo kushindwa kuwafikia wakulima wengi huko vijijini. Ni vyema Serikali ikaangalia jambo hili kwa kina kwa kuongeza Maafisa Ugani wa kutosha katika Halmashauri zetu kwa kuwa maafisa hawa ni kiungo muhimu katika kuyafikia maendeleo ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nieleze masikitiko yangu juu ya mgao mdogo wa ruzuku ya pembejeo kwa Mkoa wa Singida kwa msimu wa mwaka 2016/2017 ambapo Serikali ilitupa tani 20 za mbegu ya mahindi na tani 100 za mbolea ya kupandia/kukuzia ambayo ni sawa na asilimia 0.29 ya mbolea kwa mahitaji ya mkoa mzima. Hiki ni kidogo sana kwa mkoa kwani mahitaji yetu ni kuanzia tani 33,000 hadi tani 40,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Singida ni miongoni mwa mikoa inayolima mazao ya mafuta, kwa Mikoa ya Pwani ni nazi, kwa Mkoa wa Kigoma ni mawese, kwa Singida na Dodoma ni alizeti lakini Serikali haijalitaja zao hili kama zao la kimkakati ili tija iweze kuonekana na hata mpango wa SPDA II haujatilia mkazo zao hili. Kwa msimu uliopita, takribani tani 58,000 ziliuzwa nchini Congo ambazo ziliingiza zaidi ya shilingi bilioni 1.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iwapo zao hili litatiliwa mkazo, uzalishaji utaweza kuongezeka lakini wakulima hawa wa alizeti wamesahaulika, wengi hawana mbinu mpya bado wanatumia mbinu za zamani ambazo husababisha uzalishaji mdogo hata viwanda vilivyopo vya kuchakata alizeti havina viwango vyenye ubora wa kutosha. Iwapo Serikali itaviendeleza viwanda hivi vitaweza kuzalisha mafuta mengi yenye ubora wa kuweza kuuzwa ndani na nje ya nchi. Ifike wakati sasa Serikali iwatazame wakulima wa zao la alizeti kwa kuwapa mbegu bora za F1, utaalam wa kilimo cha kisasa na ruzuku ya pembejeo ili kukiboresha kilimo hiki cha alizeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni mfumo wa manunuzi wa pamoja wa pembejeo (bulk procurement). Naipongeza Serikali kwa kubuni mfumo huu kwani utamaliza matatizo yaliyopo katika mfumo wetu wa sasa. Wakulima wetu wameteseka sana kwa kulanguliwa na kuuziwa pembejeo zisizo na viwango kama ilivyotokea msimu uliopita wakulima wa pamba Singida walipata hasara kubwa. Hapa naishauri Serikali kuangalia mambo matatu kwa kina ili kufanikisha mfumo huu. Moja, ni udhibiti wa bei, ubora wa pembejeo na mahitaji kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nashauri Serikali kujikita katika kilimo cha umwagiliaji na hasa katika Mkoa wa Singida ili wananchi wa mkoa huu waweze kulima kwa msimu wa mwaka mzima kwa kuwa jiografia yake ni mkoa wenye ukame.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri na timu yake.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mezani. Kipekee nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na afya njema. Nitajielekeza moja kwa moja kuchangia zao la alizeti pamoja na kitunguuu endapo muda utatosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Singida ni Mkoa unaoongoza kwa kuzalisha zao la alizeti. Serikali imekuwa ikisema kwamba zao hili ni la kimkakati lakini mkakati huu upo katika maandishi na wala si kwa vitendo. Niiombe sana Serikali mkakati huu wa kuzalisha zao la alizeti uwepo kwa vitendo ili wananchi wa Mkoa wa Singida waweze kunufaika na ukulima wenye tija wa zao hili la alizeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mkoa wa Singida wamekuwa wakikabiliwa na changamoto nyingi katika kulima zao hili la alizeti. Hivi majuzi kulikuwa na uhaba mkubwa wa mafuta ambayo yanatokana na zao la alizeti. Kama Serikali ingetoa kipaumbele basi nina uhakika kabisa zao hili la alizeti lingeweza kumaliza changamoto kubwa ya uzalishaji wa mafuta lakini pia lingeweza kukuza uchumi wa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Singida ndiyo inayoongoza kwa kulima alizeti bora kabisa Afrika ya Mashariki na Afrika ya Kati lakini kilimo hiki cha alizeti kimekuwa hakipewi umuhimu. Niiombe sana Serikali iweze kufungua milango kwa wakulima wetu kwani wakulima wengi wamekata tamaa na hata kwa msimu uliopita, alizeti hii imezalishwa kwa kiwango cha chini sana. Kwa kuwa, Serikali inayo dhamira nzuri ya kuanzisha mashamba ya kimkakati, basi itenge maeneo ambayo sasa yatakwenda kufungua fursa za uzalishaji wa kilimo hiki cha alizeti katika halmashauri zetu kwani halmashauri za Mkoa wa Singida zote zinalima zao hili la alizeti, zikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Mkalama, Ikungi, Manyoni pamoja na Iramba. Naishauri sana Serikali iweze kufungua milango kwa wawekezaji waje kuwekeza katika zao hili la alizeti ili sasa tija iweze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa katika zao letu hili la alizeti ni uzalishaji wa mbegu. Niiombe sana Serikali iweze kutoa kipaumbele kwa taasisi zetu hizi za ASA pamoja na TARI, ambazo zimekuwa zikizalisha mbegu aina ya records ziweze kupewa bajeti ya kutosha ili ziweze kuzalisha mbegu hizi na kuweza kumaliza changamoto hii. Wakulima wetu wamekuwa wakinunua mbegu hii kwa Sh.3,500 kwa kilo lakini imekuwa ikizalishwa tu kwa tani 500 kwa mwaka wakati viwanda vyetu vinaweza kuzalisha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Aysharose Mattembe.

MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia 100.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, wote tunatambua kuwa maji ni uhai katika maisha ya mwanadamu, maji ni maendeleo, maeneo ambayo hakuna maji hakuna maendeleo na asilimia kubwa ya shughuli za kijamii na kiuchumi zinategemea uwepo wa maji. Naishauri Serikali kuangalia uwezekano wa kuongeza tozo ya maji kwa lita moja ya petroli na dizeli kutoka Sh.50/= hadi Sh.100/= ili kutunisha Mfuko wa Maji ambao umekuwa mkombozi mkubwa wa maendeleo ya miradi ya maji maeneo mengi nchini lakini wanufaika wengi wamekuwa ni wale wanaoishi mijini. Nashauri Serikali itazame zaidi maeneo ya vijijini angalau kupeleka 70% ya makusanyo ya tozo ya Mfuko wa Maji maeneo ya vijijini ambapo ndio kwenye shida kubwa ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama maji yanapatikana wakati wote wanawake wa Mkoa wa Singida ambao ni wachapakazi na wabunifu wanaweza kutumia fursa hii kwa kulima mazao ya chakula na biashara kwa mwaka mzima. Hata hivyo, kwa Mkoa wa Singida mambo yamekuwa sivyo ndivyo pamoja na adha kubwa wanayoipata wananchi wa Singida kutokana na ukosefu wa maji safi na salama na changamoto nyingi za maji katika Mkoa wa Singida bado bajeti ya miradi kwa mwaka huu wa fedha 2017/2018 imepunguzwa ambapo tumetengewa shilingi bilioni 4.7 tofauti na mwaka wa fedha 2016/2017 ambapo tulipewa shilingi bilioni 6.7 jambo hili si sawa. Naiomba Serikali yangu kuangalia upya bajeti hii na kuiongeza kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mosi, Singida ipo katikati ya nchi na ni mkoa unaokuwa kwa kasi, unategemea vyanzo vya maji ya visima virefu na vifupi ambavyo maji yake ni ya chumvi na hata hivyo hayakidhi viwango vya mahitaji. PiIi, hali ya hewa ya Mkoa wa Singida ni kame hivyo ingetakiwa kupewa kipaumbele katika miradi mikubwa ya maji. Maeneo mengi ya Mkoa wa Singida yanakabiliwa na ukosefu wa maji safi na salama na tatizo hili limekuwa ni la muda mrefu licha ya Serikali kuambiwa tatizo hili mara kwa mara bila kulipatia ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi Mkoa wa Singida hususan wanawake wameteseka sana na adha kubwa ya ukosefu wa maji. Ni vyema Serikali ikasikia kilio cha wakazi wa Mkoa wa Singida na kuchukua hatua madhubuti na za haraka kumaliza tatizo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu imejaliwa kuwa na mito mikubwa, maziwa na bahari, ni lini tutatumia kikamilifu rasilimali hizi? Ni kwa nini tusitumie vizuri uwepo wa Ziwa Manyara ambalo lipo umbali wa kilomita 177 kuvuta maji kuja Singida ama kutoka Ziwa Viktoria kupitia Tabora, Nzega, Igunga hadi Singida? Tutaendelea kuwatesa wanawake wa Mkoa wa Singida mpaka lini na kuhatarisha ndoa zao kwa kutoka usiku kufuata maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kukabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji safi na salama bado kuna changamoto nyingi zinazoikabili Idara ya Maji ya Mkoa wa Singida (SUWASA). Changamoto hizo ni ukosefu wa vitendea kazi, uhaba wa watumishi na ucheleweshaji wa fedha za utekelezaji wa miradi ya maji. Ni jambo la kushangaza mkoa ambao unatakiwa kupewa kipaumbele kutokana na jiografia yake lakini unaongoza kwa uhaba wa watumishi. Kuna wahandisi 12 tu lakini wanaohitajika ni wahandisi 28, mafundi sanifu wanaotakiwa ni 52 ila waliopo ni 20 na kwa kuwa kazi nyingi za miradi ya maji ni field work sasa kwa mazingira haya tutafanikisha?

Mheshimiwa Naibu Spika, mkoa mzima hauna GPS machine, kuna magari matatu ambayo yapo juu ya mawe na pikipiki moja tu. Je, kwa staili hii kazi zinaweza kufanyika kweli kwa ufanisi? Mkoa wa Singida unahitaji crane truck 15, computer nane, GPS machine sita, pikipiki 10 ili kuwezesha maofisa wa maji kufika wilayani na vijijini kutatua kero ya maji na hata Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji- Singida (SUWASA) hana gari. Naomba Serikali ipeleke vitendea kazi ili kuwawezesha wananchi wa Mkoa wa Singida kupata huduma bora za maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya miradi ambayo tuliamini ingekuwa mkombozi wa wananchi wa Singida lakini mingi imekwama kukamilika kutokana na changamoto mbalimbali zikiwemo ukosefu na ucheleweshwaji wa fedha kutoka Serikalini. Kuna miradi ambayo tayari imeshafanyiwa usanifu ya Manyoni na Kiomboi lakini haijapata fedha mpaka sasa. Miradi mingine ni ya Mkwa, Iyumbu, Ulyampiti na Sepuka ambapo inasubiri fedha toka Serikalini. Niishauri Serikali ipeleke fedha kwa wakati ili kukamilisha miradi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Singida Vijijini na Wilaya ya Manyoni ni wilaya zinazokabiliwa na upungufu na ukosefu mkubwa wa maji safi na salama na wakazi wake wanategemea zaidi maji ya visima virefu na vifupi. Mfano, Wilaya ya Singida visima vyake vingi ni vibovu na miundombinu yake ni chakavu ambayo haijafanyiwa ukarabati kwa muda mrefu kutokana na ukosefu wa fedha na kutopelekwa fedha hizo. Ukarabati wa miradi ya visima vifupi na virefu ambavyo vilikuwa vinafadhiliwa na fedha za WDPS kutoka Serikali Kuu, fedha hizi kwa muda mrefu hazijaletwa. Sasa ni vyema Serikali ikaangalia uwezekano wa kupeleka fedha hizo ili wananchi wa Mkoa wa Singida wa Wilaya ya Singida Vijijini waweze kupata huduma bora za maji ya uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuelezea changamoto hizi hapo juu, naunga mkono hoja na nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji, Naibu Waziri wa Maji, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara ya Maji kwa namna ambavyo wanashughulika kutatua kero ya maji pamoja na changamoto zinazoikabili Wizara yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijalia uzima na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako tukufu. Naishukuru Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri wanayoendelea kuifanya ya kuwaletea wananchi maendeleo ya haraka na yenye tija. (Makofi)

Pili, nampongeza sana Waziri wa Afya na timu yake kwa juhudi kubwa wanayofanya kuboresha huduma za afya na upatikanaji wa dawa ambapo hapo awali ilikuwa ni changamoto kubwa na kero kubwa kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na bajeti iliyowasilishwa mbele ya Bunge lako tukufu, bado kuna changamoto kubwa eneo la afya la mama na mtoto. Takwimu zinaonesha kwa mwaka 2004/2005 vifo vya mama wajawazito vilikuwa 578 kati ya vizazi hai 100,000; mwaka 2009/2010 vilishuka na kufikia 434 kati ya vizazi hai 100,000; lakini mwaka 2015/2016 vifo vya akina mama wajawazito vilipanda hadi kufikia 556 kutoka vizazi hai 100,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa takwimu hizi, bado tuna kazi kubwa ya kufanya ili kupunguza vifo vya wakina mama wajawazito. Ikumbukwe kwamba tulijiwekea malengo ifikapo mwaka 2020 tuwe tumepunguza vifo hivi viwe vimefikia 292 katika vizazi hai 100,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iongeze nguvu katika kuajiri wataalam hasa katika Kitengo cha Afya ya Mama na Mtoto lakini pia katika kada zote za afya, kwani kwa Mkoa wetu wa Singida tuna uhaba mkubwa sana wa watumishi katika kada ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuajiri wataalam hao, tuende sambamba na kuleta vifaa tiba katika wodi zetu za wazazi, kwani vilivyopo ni chakavu na havitoshelezi mahitaji. Katika Mkoa wa Singida jiografia yake ni ngumu sana na inahitaji ambulance nyingi za kutosha ili kuepuka vifo vya akina mama na watoto na kuwafikia haraka sehemu za kutolea huduma kwa wakati. Inasikitisha sana, baadhi ya Hospitali za Wilaya na Vituo vya Afya vya Ikungi, Manyoni na Itigi havina kabisa magari ya kubebea wagonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutarajie nini kwa mama ambaye tayari ameshashikwa na uchungu wakati hakuna usafiri wa kumfikisha katika kituo cha kutolea huduma? Mheshimiwa Ummy dada yangu mpendwa najua wewe ni msikivu na ni mama wa wanawake wanyonge na suala hili nimekuwa nikikuletea mara kwa mara kwamba Hospitali yetu ya Mkoa wa Singida haina kabisa gari ya kubebea wagonjwa, hivyo nakuomba unisaidie ili tuweze kupata magari ya kubebea wagonjwa na pia tuweze kusaidia kuokoa vifo vya akina mama wajawazito na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie Hospitali yetu ya Rufaa ya Mkoa wa Singida. Hospitali hii imejengwa takribani miaka kumi iliyopita, lakini mpaka sasa haitoi huduma. Vitengo vinavyotoa huduma ni vitengo vitatu tu; Kliniki ya Uzazi na Mtoto, Kliniki ya Ngozi na Kliniki ya Wagonjwa wa Kisukari. Sasa inawezekana vipi hospitali yenye hadhi ya kuitwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa iweze kuhudumia vitengo vitatu tu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inasikitisha sana hata baadhi ya majengo yameshaanza kuchakaa. Sasa ni kwa nini Serikali haitoi fedha za kutosha ili Hospitali hii ya Rufaa iweze kukamilika na kuanza kutoa huduma na hata hatimaye kupunguza msongamano katika hospitali zetu za Wilaya na vituo vyetu vya afya? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba wakati Waziri wa Afya atakapokuja kufanya majumuisho, anipe commitment ya Serikali ni lini Hospitali hii ya Rufaa itakamilika?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hospitali yetu ya mkoa haina Madaktari Bingwa wa kutosha; madaktari waliopo ni sita tu, wakati ikama inahitaji kuwa na madaktari 33. Naomba Serikali iwaonee huruma…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na mengine nitayaleta kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ya bajeti ya Wizara ya Afya. Namshukuru Mungu kwa kunijalia zawadi ya uhai na afya njema. Pia nampongeza sana Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Naibu Waziri wake Mheshimiwa Dkt. Mollel na Katibu Mkuu Dkt. Abel Makubi na watendaji wote wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri ya kuhakikisha wanapata huduma bora za afya, nawapongeza sana, Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Spika, nieleze kwa masikitiko makubwa juu ya kusuasua kwa ujenzi wa hospitali yangu ya rufaa ya mkoa ambao ujenzi wake umekuwa ni wa muda mrefu kwa zaidi ya miaka13 hadi sasa hospitali hii haijakamilika.

Mheshimiwa Spika, majengo haya ambayo yalijengwa miaka iliyopita yameshaanza kuchakaa na yatahitaji bajeti nyingine kwa ajili ya ukarabati hivyo kutokuwa na thamani ya ujenzi wa hospitali hiyo.

Mheshimiwa Spika, naishukuru Serikali kwa kuendelea kututengea fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali yetu ya rufaa lakini fedha hizi zimekuwa hazitoshi. Ninaiomba Serikali itutengee fedha za kutosha ili hospitali hii ya rufaa iweze kukamilika, endapo hospitali hii itakamilika itakuwa ni msaada mkubwa sana kwa wananchi ambao wengi hawamudu gharama za matibabu kwenye hospitali za rufaa za mikoa ya jirani hususani wanawake waishio pembezoni. Ninaomba Mheshimiwa Waziri Ummy atapokuja ku-wind unipe commitment ya Serikali ni lini hospitali hii ya rufaa ya Singida ni lini itakamilika?

Mheshimiwa Spika, pia hospitali hii ya rufaa ya mkoa inakabiliwa na uhaba mkubwa wa vifaa tiba, watumishi wakiwemo madaktari bingwa, tuna madaktari bingwa sita tu na miongoni mwa hao wapo masomoni. Ninaiomba Serikali ituletee madaktari bingwa wa kutosha akiwemo daktari bingwa wa watoto ili wananchi wetu waweze kupata huduma za kibingwa ndani ya mkoa wao.

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Serikali kwa kutujengea hospitali za Wilaya ya Mkalama, Singida DC na Ikungi, lakini hospitali hizi hazina vifaa tiba, watumishi na dawa za kutosha.

Mheshimiwa Spika, uwepo wa majengo haya mazuri bila ya vifaa tiba na wataalam ni kazi bure, mfano hospitali ya Wilaya ya Mkalama, kwa mwaka wa fedha ulioisha 2021/2022 tulitengewa fedha shilingi milioni 500 kwa ajili ununuzi wa vifaa tiba, lakini ni vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 77 tu ndivyo vilivyoletwa katika hospitali hii, jambo hili linasikitisha sana, fedha ipo lakini ni kwa nini MSD hawaleti vifaa tiba? Wilaya hii pia ina uhaba mkubwa wa watumishi 607. Naomba tuletewee vifaa tiba, watumishi na dawa za kutosha katika hospitali zetu za Wilaya, vituo vya afya na zahanati za Mkoa wa Singida ili malengo mazuri ya Serikali yaweze kutimia.

Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi.

Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na afya njema. Naipongeza Serikali kwa bajeti nzuri waliyoiwasilisha mbele ya Bunge lako tukufu kwa mustakabali wa elimu ya vizazi vya sasa na vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iwapo bajeti hii itatekelezwa ipasavyo tuna imani kubwa kwa Watanzania kunufaika na mfumo wa elimu ya sasa. Hata hivyo kuna maeneo ambayo yanahitaji kutiliwa mkazo ili kuhakikisha tunayaboresha na pia vilevile kukuza kiwango cha elimu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mafanikio makubwa ambayo yamefikiwa kwa kipindi kifupi katika sekta ya elimu lakini bado kuna changamoto ambazo Serikali inatakiwa kuzipatia ufumbuzi. Eneo la kwanza ambalo ningependa Serikali ilifanyie kazi kwa haraka ni uhaba wa walimu na miundombinu isiyokidhi mahitaji kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi nchini ukiwemo Mkoa wangu wa Singida kuna uhaba mkubwa wa nyumba za walimu. Kwa mfano, kwa Mkoa wa Singida pekee una uhaba wa nyumba za walimu 1,986 jambo hili linasababisha walimu wengi kuishi uraiani ambako hakuna utulivu na pia linawavunja moyo wa kuweza kuwafundisha wanafunzi wetu inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kitabu cha hotuba ya Waziri wa Elimu ukurasa wa 89, TEA imetenga shilingi bilioni 9.7 kwa ajili ya kazi mbalimbali zikiwemo ujenzi wa nyumba za walimu, mabweni pamoja na matundu ya vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Mkoa wa Singida upewe kipaumbele kwani una uhaba mkubwa wa nyumba za walimu, vyumba vya madarasa na matundu ya vyoo. Vile vile Mkoa wa Singida unakuwa kwa kasi sana na Jiografia yake ni ngumu na maeneo mengi hayafikiki kwa urahisi. Kwa mfano shule ya msingi ya Mangoli iliyopo Jimbo la Manyoni Mashariki ipo umbali wa kilometa 137 kutoka Manyoni Mjini. Shule hii ni nyumba moja ya mwalimu yenye vyumba viwili, imepelekea kuvunjika kwa ndoa za walimu hao kwani upande mmoja wanalala wake zao na upande mwingine wa nyumba hiyo wanalala walimu hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali hii kweli walimu wetu wataweza kuwafudisha wananfunzi kwa umakini?

Mheshimiwa Ndalichako nakuomba ulichukulie suala hili kwa umakini mkubwa kuweza kuhakikisha nyumba za walimu zinapatikana kwa wingi. Pia naishauri Serikali kuharakisha ujenzi wa nyumba za walimu, mabweni pamoja na matundu ya vyoo na uende sambamba na ujenzi wa vyoo unaozingatia sehemu za kujihifadhia wanafunzi wa kike wanapokuwa katika siku zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine lenye changamoto kubwa ni uhaba wa walimu na hasa wa masomo ya sayansi katika shule za sekondari. Kwa kuwa nchi yetu kwa sasa inaelekea katika uchumi wa viwanda, na tunahitaji kuzalisha wataalam wengi ambao watakuja kuviendesha viwanda hivi, ningeomba Serikali ilichukulie jambo hili kwa umakini mkubwa. Kwa mfano kwa Mkoa wa Singida tu una uhaba wa walimu wa sayansi 660 katika shule zetu za sekondari na kwa upande wa shule za msingi kuna uhaba wa walimu 3,947 kwa masomo ya sayansi na sanaa. Naishauri Serikali iangalie utaratibu wa uhakika wa kuzalisha walimu ili kwenda sambamba na mipango ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa mkakati wake wa kusambaza vifaa vya maabara katika shule zetu za sekondari, ni mpango mzuri na ninaomba uwe endelevu. Kwa kuwa kwa mwaka 2017/2018 kuna shule za sekondari kwa Mkoa wa singida ambazo hazijapata vifaa vya maabara ninaomba Serikali iangalie jambo hili basi ipeleke vifaa vya maabara katika shule zetu za sekondari kwa Mkoa wa Singida. Ninawapongeza sana wananchi wa Mkoa wa Singida kwa kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa maabara na pia vilevile ninaiomba Serikali iweze sasa kuona umuhimu wa kumaliza maabara zile ambazo zimefikia maeneo ya lenter.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba Serikali iuangalie kwa jicho la tatu Mkoa wa Singida kwani una uhaba mkubwa sana wa vyumba vya madarasa. Kwa shule za sekondari tu kuna uhaba wa vyumba 122 na kwa shule za msingi kuna upungufu wa vyumba vya madarasa 4,849.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitumie fursa hii kuwashukuru Kampuni ya Tanga Cement ambao wamekuwa msitari wa mbele kusaidia jamii kuboresha miundombinu ya elimu. Ahsanteni sana Tanga Cement na nawaomba muendelee na moyo huo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naipongeza Seriakli kwa mkakati mpya wa kuwasaidia vijana ambao wako mitaani kupata mafunzo ya ufundi kwa njia ya vocha kupitia Bodi ya Mikopo na Mkoa wangu wa Singida ni miongoni mwa Mikoa minne ambayo imeanza kutekeleza mpango huo. Lakini changamoto iliyopo ni kwamba fedha za mafunzo ya ufundi kwa vitendo kutoka bodi ya mikopo hadi sasa bado hazijapelekwa. Ningeiomba Serikali ifanye haraka kupeleka fedha hizo kwa kuwa vijana hao zaidi ya 200 wapo stranded na sasa hawasomi kwa vitendo masomo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nawapongeza Mheshimiwa Ndalichako, Mheshimiwa Ole Nasha na timu yake kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuendelea kuboresha miundombinu ya elimu. Nawapo moyo, endeleeni na moyo huo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba hii muhimu kwa maendeleo ya Watanzania. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kuwapongeza sana Waziri wa Maji, Mheshimiwa Engineer Kamwelwe, Naibu wake, Mheshimiwa Aweso na timu nzima kwa kufanya kazi nzuri ya kuhakikisha Watanzania wanapata huduma muhimu ya maji. Nawapongeza sana na nawatia moyo waendelee kufanya kazi hiyo pamoja na changamoto zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na wenzangu kusema kwamba maji ni uhai, shughuli nyingi zinategemea uwepo wa maji. Viwanda, kilimo, mifugo na binadamu wote uhai wake ni maji. Waathirika wakubwa wa ukosefu wa maji ni wanawake, wanawake hawa wamekuwa wakitembea umbali mrefu kutafuta maji na hivyo kutokushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji mali na wakati mwingine kuhatarisha ndoa zao kwani hutoka usiku sana kutafuta maji hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Maji inamtaka mwananchi kutembea umbali wa mita 400 ili kuweza kuyapata maji. Kwa Mkoa wa Singida maeneo mengi ya vijijini imekuwa ni kinyume, wanatembea umbali mrefu hasa wanawake waishio maeneo ya vijijini kuyasaka maji. Kwa kuwa tunaelekea Tanzania ya viwanda, niombe sana maeneo haya ya vijijini yaweze kupatiwa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida ni miongoni mwa mikoa ambayo inakua kwa kasi, lakini inapata mvua kwa msimu mmoja kwa mwaka. Hivyo basi naiomba Serikali kuja na mkakati mahsusi wa kuchimba mabwawa ya kuweza kuhifadhi maji kwa mwaka mzima ili kuwawezesha wanawake ambao ni wakulima wazuri wa mazao ya biashara na chakula kuweza kulima kwa muda wa mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali kwa kutupatia fedha katika miradi ya maji ya vijiji kumi vya Mbwasa katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni. Niiombe iongeze juhudi zaidi kupeleka fedha katika mpango wa pili wa ukamilishaji wa mradi huo.

Pia naishukuru sana Serikali kwa kutupelekea fedha katika Mradi wa Maji wa Uliyampichi uliopo Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, lakini changamoto iliyopo katika mradi huo ni kwamba hakuna pump na fedha za kuweza kuunganishwa na umeme ili uweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida Vijijini kuna Mradi wa Maji wa Kijota, lakini mradi huo umekuwa ukitumia pump ya dizeli ambayo kwa sasa imeharibika. Niiombe sana Serikali iweze kupeleka fedha kiasi cha shilingi milioni 94.6 ili basi waweze kutumia pump ambayo itatumia umeme na kwa kuwa kuna miundombinu ya umeme mradi huo uweze kuunganishwa na umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipindi kilichopita nilikuwa Mjumbe wa Kamati ya LAAC na kazi kubwa tuliyokuwa tukifanya ni kukagua miradi ya maendeleo na mingi ilikuwa ni ya maji, lakini changamoto kubwa tulizokuwa tukikutana nazo ni miradi mingi ya maji kutokukamilika kwa wakati au utakuta miradi mingine imekamilika lakini haifanyi kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninao mfano hai kwa Mkoa wangu wa Singida wa Mradi wa Unyanga na Mradi wa Mchama B, ni miradi ambayo imetumia mamilioni ya fedha za walipa kodi lakini haifanyi kazi. Namuomba Waziri wakati wa majumuisho atuambie ni kwa nini miradi ya maji ambayo imetumia fedha nyingi za walipa kodi haifanyi kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Itigi unakua kwa kasi lakini hauna kabisa mtandao wa maji. Naiomba Serikali iangalie vile visima ambavyo tayari vimechimbwa basi ipeleke fedha za kutosha ili kuweza kuunganisha miundombinu na mji huo uweze kupata maji ya uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya machache, nakushukuru sana, mengine nitachangia kwa maandishi, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema kubwa ya kutuwezesha kuwa hapa kwa ajili ya kupigania maslahi mapana ya Taifa letu. Aidha, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa maandalizi ya bajeti hii yenye maono makubwa yanayoelekea kustawisha ukuaji wa uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nimeisoma bajeti iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri mbele ya Bunge lako tukufu na nimeona nichangie mambo machache; moja ni suala la ulipaji kodi; nchi yetu inao uwezo mkubwa wa kujiendesha kibajeti kwa kuwa ina maeneo mengi ya kukusanya kodi hususan kupitia nyanja mbalimbali za biashara, za uzalishaji, lakini jambo kubwa linalokosekana ni elimu, utayari, sheria na msukumo wa uhakika katika suala la ulipaji kodi. Ni ukweli usiopingika kuwa wananchi wengi hawana utayari wa kusimamia masuala ya kikodi hususan utoaji risiti, jambo hili linaturudisha nyuma.

Pili ni suala la makubaliano yasiyo rasmi katika ulipaji kodi, kumekuwa na tabia ya wafanyabiashara wasio waaminifu kufanya makubaliano ya kulipa kodi nje ya utaratibu na kuwanufaisha watumishi wachache wasio waaminifu wa mamlaka za mapato huku wao wakilipa kiasi kidogo cha kodi. Kupitia mwenendo huu Serikali inapoteza mapato mengi na kupelekea uhafifu wa kutekeleza malengo ya Serikali.

Tatu ni saula la mikopo kwa wazawa, kumekuwa na mwenendo wa wawekezaji au wataalam wazawa kukosa sifa za kiushindani katika masuala ya uwekezaji kutokana na kutokuwa na mitaji ya kutosha. Ni muhimu Serikali iweke sera ya kipaumbele juu ya wazawa kupatiwa mitaji kupitia mikopo inayotolewa na mabenki yetu. Kwa kuweka umuhimu wa jambo hili kundi la wanawake ni moja ya eneo ambalo Serikali inaweza kuwekeza mtaji na kuwa na uhakika wa matokeo chanya.

Mheshimiwa Spika, mwisho ni sera ya uwekezaji wa viwanda vya ndani na kilimo katika mazao ya kimkakati hususan chikichi, ngano na alizeti, ni lazima Taifa letu litoke kwenye mfumo wa kutegemea bidhaa kutoka nje na badala yake tuwe wazalishaji ambao kazi yetu itakuwa kutafuta masoko ikiwa tumeshajitosheleza. Hivyo nashauri maeneo haya muhimu yapewe kipaumbele ili kuweza kujitegemea kupitia soko la ndani na kuokoa fedha nyingi inayokwenda nje kwa ajili ya kuagiza bidhaa ikiwemo mafuta na ngano.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitapenda kuchangia katika maeneo matatu; eneo la kwanza ni uhaba wa watumishi. Suala hili limekuwa likiathiri kwa kiasi kikubwa utoaji wa huduma kwa wananchi na kupunguza ufanisi katika utendaji wa kazi katika halmashauri zetu na limekuwa ni la muda mrefu hata kabla ya uhakiki wa watumishi hewa na wasiokuwa na sifa, malalamiko yalikuwa ni makubwa na baada ya zoezi hilo likaongeza zaidi makali ya changamoto hii ya uhaba wa watumishi. Mfano, katika Mkoa wangu wa Singida, Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama pekee ina upungufu wa watumishi 462 katika Sekta ya Afya; Manyoni uhaba wa watumishi 446; Itigi watumishi 269 na Ikungi 822.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takwimu hizi unaweza kuona jinsi gani changamoto hii ilivyo kubwa. Naishukuru Serikali kwa kukubali ushauri na kuwarejesha watumishi kazini kulingana na sifa zao, lakini naishauri ni vyema sasa ikaja na mikakati ya makusudi ya kuajiri watumishi wengi ili kuziba upungufu uliopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo napenda kulichangia ni ucheleweshwaji wa fedha za shughuli za maendeleo katika halmashauri zetu. Suala hili limesababisha kukwama kwa miradi mingi au kutokukamilika kwa miradi kwa wakati na kuisababishia Serikali hasara na kwa upande wa wananchi imekuwa ni kero kubwa kusubiri mradi kwa muda mrefu na hivyo kuwakosesha huduma muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba bajeti yetu hutegemea makusanyo ya mapato kwa mwezi, lakini uhalisia wa kiasi cha fedha tunachokiidhinisha katika shughuli za maendeleo kinatofautiana kwa kiasi kikubwa cha fedha zinazopelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ni vyema sasa ikajitathmini na kurekebisha hali hii, miongoni mwa mikakati ya kujirekebisha na kujitathmini ni kupeleka fedha zlizobaki za miradi ya maendeleo katika Mkoa wangu wa Singida. Ni vyema Serikali ikaimarisha ukusanyaji wa mapato kwa njia ya kisasa (kielektroniki) ikiwemo elimu ya mlipakodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo napenda kulichangia ni asilimia 10 ya mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana zitokanazo na mapato ya ndani katika halmashauri zetu. Imekuwa ni kawaida kwa Maafisa Masuuli kutokupeleka kwa makusudi au kutokupeleka kwa wakati asilimia 10 ya mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana. Muda uliopita nilikuwa ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC na tatizo hili tumekuwa tukikutana nalo kila mara tulipokwenda kufanya ukaguzi katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kwamba wanawake na vijana hawa ndio makundi muhimu na nguvu kazi ya Taifa katika kukuza uchumi lakini wengi wao hawana dhamana ya kukopa katika mabenki na taasisi za fedha kwa kutopeleka asilimia 10 ya mikopo kwa vikundi vya vijana na wanawake ni kuwakosesha fursa ya kukua kiuchumi. Naishauri Serikali ije na mikakati mahususi ambayo itawabana Maafisa Masuuli waweze kupeleka asilimia 10 za mikopo kwa vikundi vya vijana na wanawake kwa kiasi kikubwa kinachotakiwa na kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishauri Serikali iimarishe Idara ya Maendeleo ya Jamii ili iweze kufanya kazi yake ipasavyo kwa kukaa na makundi haya na kuwaelimisha juu ya mikopo hiyo hatimaye iweze kuleta tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nawapongeza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo na Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Kandege na Mheshimiwa Kakunda kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya ya kuwaletea wananchi maendeleo; nawatia moyo waendelee na kasi hiyohiyo ya utendaji wa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba hii muhimu ya maji kwa maendeleo ya Watanzania. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya chama changu kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuwaletea Watanzania maendeleo. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais, amekuwa na ziara ndefu akihamasisha maendeleo, hakika tunamwombea heri, baraka na nguvu katika kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Maji Profesa Mbarawa, Naibu wake Mheshimiwa Aweso, Katibu Mkuu, Kitilya Mkumbo, pamoja na watendaji wote kwa hotuba nzuri, hotuba ambayo inatoa mwelekeo wa kumtua ndoo mwanamke kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ndiyo kila kitu. Maji ni uhai, maji ni maendeleo, maji ni uchumi, lakini maji haya yamekuwa yakileta madhara makubwa, mfarakano na kusababisha ndoa nyingi kuvunjika na kuwafanya wanawake wengi kutokushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wangu wa Singida unakabiliwa na changamoto kubwa ya ukosefu wa maji safi na salama, hususan maeneo ya vijijini na hii ni kutokana na jiografia yake. Jambo kubwa la kusikitisha ni kwamba, hata miradi mikubwa inayopangwa kutekelezwa katika Mkoa wa Singida imekuwa ikisuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Mradi wa Maji Kitinku, Lusilile katika Wilaya ya Manyoni, uliibiliwa chini ya mpango wa Matokeo Makubwa Sasa na ulianza kutekelezwa mwaka 2013, lakini hadi leo ni miaka sita mradi huu haujakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Waziri atakapokuja kufanya majumuisho atuambie, ni lini fedha za kutosha zitapelekwa kwa wananchi wa Manyoni ambao wanausubiri mradi huu kwa hamu kubwa na ni vijiji kumi vitakavyonufaika. Vijiji hivi ni Kintinku, Lusilile, Maweni, Chikuyu, pamoja na vijiji vingine ambavyo vipo karibu katika maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kutupa miradi mikubwa miwili ya maji ya mtandao wa bomba katika Jimbo la Ikungi Magharibi. Miradi hii ni ya Ighuka na Mtunduru, lakini niombe sana, sana Serikali ipeleke fedha za kutosha ili miradi hii iweze kukamilika kwa wakati kwa sababu wananchi wa Jimbo la Ikungi Magharibi wanapata tabu sana ya ukosefu wa maji safi na salama. Pia naishukuru Serikali kwa kutupa vibali vya kuchimba visiwa 20 kwenye Jimbo la Ikungi Magharibi pamoja na Ikungi Mashariki. Naomba vibali hivi viende sambamba na kutupa fedha za kutosha ili wananchi waondokane na adha ya ukosefu wa maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa maji katika Mkoa wangu wa Singida hususan maeneo ya vijijini bado ni duni sana na vijiji vingi bado havina huduma ya maji safi na salama. Mfano Jimbo la Singida Kaskazini Vijiji vya Mitula, Migugu, Ughandi B, Misinko, Mwighanji havina kabisa mtandao wa maji, maji wanayotumia ni maji ya malambo na unapofika wakati wa kiangazi, maji haya yanakauka na wananchi wanapata tabu kubwa sana ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ningependa kuchangia ni ukosefu mkubwa wa vitendea kazi yakiwemo magari, pamoja na watumishi wa Idara za Maji. Naishauri Serikali iangalie jambo hili kwa jicho la tatu; Wilaya zangu zote za Singida ikiwepo Mkalama, Manyoni, Ikungi, Iramba na Singida Vijijini wapate watumishi pamoja na magari na vitendea kazi vya kutosha. Naipongeza na kuishukuru Serikali kwa kutupa Mamlaka za Maji katika Miji Midogo ya Ikungi, Mkalama na Itigi. Tayari Bodi zimeshaundwa na mapendekezo yameshapelekwa Wizarani. Naiomba Serikali basi iharakishe upatikanaji wa bibali hivi, naamini kwamba Mamlaka hizi za Maji zitaweza kusaidia sana upatikanaji wa maji katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala lingine ambalo ningependa kulichangia; kuna changamoto kubwa sana ya ukosefu wa maji katika Taasisi za Elimu na Afya. Watoto wetu wa shule wamekuwa wakitumia muda mrefu sana kuhangaika kutafuta maji na unategemea jambo gani la ufaulu iwapo watoto hao wanatumia muda mwingi kutafuta maji. Pia watoto wanapofika siku za hedhi, watoto wa kike wanataabika sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kubwa la kusikitisha ni kwamba wanawake wajawazito wanapokwenda kujifungua wanaambiwa waende na maji ni kwa sababu kwamba Taasisi hizi za Afya zinakuwa hazina miundombinu ya maji. Niombe sana pia Serikali iangalie jambo hili kwa jicho la tatu, iweke miundombinu katika shule zetu pamoja na Taasisi za Afya ili kuweza kuwapatia wananchi huduma ya maji katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii na nakushuru kwa muda ulionipatia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba hii muhimu ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima na kutuwezesha kufikia mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani. Niwatakie Waislam wote kheri ya Mfungo wa Ramadhani hususani wananchi wa Mkoa wa Singida.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya chama changu chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuwatumikia wananchi wa Tanzania. Uzalendo uchapakazi wake maono amejipambanua ni kiongozi makini na ni mfano wa kuigwa Mheshimiwa Rais endelea kuchapa kazi sisi Watanzania tuko nyuma yako na tunakuombea sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Afya dada yangu Ummy Mwalimu, Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndungulile, Katibu Mkuu bi. Zainab Chaula pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Afya hakika wanafanyakazi nzuri sana. Nimekisoma kitabu hiki cha hotuba ya afya kwa namna kilivyopangwa na kilivyochapishwa, inaonyesha viongozi wa Wizara hii wako makini sana nawapongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika afya ndiyo utajiri na afya ndiyo mtaji wa kila mwanadamu. Niipongeze sana Serikali kwa juhudi kubwa inazochukua za kuboresha huduma za afya nchini kote. Kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Singida ninaomba kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutupa zaidi ya shilingi bilioni 5 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya 11, katika wilaya zangu zote za Mkoa wa Singida tumepata Kituo cha Afya Mkalama, Iramba, Singida Manispaa, Singida Vijijini pamoja na Wilaya ya Manyoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, Namshukuru sana Mheshimiwa Rais hakika uwepo wa vituo hivi vya afya umeokoa sana vifo vya akinamama na watoto. Lakini Sera ya afya inasema kwamba kila kata iwe na Kituo cha Afya, basi niombe pamoja na uwepo wa vituo hivi vya afya jiografia ya Mkoa wangu wa Singida ni ngumu sana niombe vituo vya afya viongezwe ili wananchi waweze kupata huduma bora za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naishukuru sana Serikali kwa kutupa bilioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za wilaya, hospitali ya Mkalama na hospitali ya Singida DC. Sasa hivi ziko katika hatua ya ujenzi na mwaka huu pia katika bajeti hii tumepata hospitali kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya wilaya ya Ikungi naishukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na pongezi hizi na shukrani hizi mkoa wangu wa Singida una changamoto lukuki katika sekta ya afya. Nikianza na hospitali ya Wilaya ya Manyoni, hospitali hii ilijengwa kama kituo cha afya mwaka 1971 na ni ya muda mrefu. Kwa hiyo, majengo ya OPD limeshakuwa ni finyu na dogo, wodi ya akinababa, wodi ya watoto, wodi ya majeruhi haiendani kabisa na idadi ya watu katika wilaya hii ya Manyoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ifahamike kwamba wilaya ya Manyoni ipo katika barabara kuu ya Mkoa wa Singida na Dodoma na ajali nyingi zimekuwa zikitokea kwa hiyo inakuwa ni changamoto sana kuwahudumia wagonjwa au majeruhi inapokuwa majeruhi hawa ni wengi ninaiomba sana Serikali itupatie fedha ili tuweze kujenga hospitali mpya ya Manyoni itakayoendana sambamba na idadi ya watu kwa wilaya yangu ya Manyoni lakini pia vilevile iweze kutoa huduma bora zaidi za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu hospitali yangu ya Rufaa ya Mkoa wa Singida, hospitali hii ina changamoto nyingi na hospitali hii ilianza kujengwa mwaka 2009 ni takriban sasa miaka tisa imepita hospitali hii haijakamilika lakini jambo kubwa la kusikitisha hospitali hii ya rufaa kwa mwaka wa fedha uliopita haijatengewa fedha zozote na inatoa huduma katika maeneo mawili ipo hospitali ya rufaa ambayo ni ya zamani, ipo katika Kata ya Ipembe, lakini pia hospitali ya rufaa ambayo ni mpya iliyoko katika Kata ya Mandewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa jambo hili linapelekea kwa kweli ugumu katika uendeshaji wa hospitali hizi mbili kwa wakati mmoja. Nimuombe Mheshimiwa Waziri najua ni msikivu na ananisikia ifike wakati sasa zitengwe fedha za kutosha ili kumalizia ujenzi wa hospitali hii.

Mheshimiwa dada yangu Ummy ninakuomba sana kwa kuwa sasa imepelekea bajeti ndogo ambayo tunaipata kulipia bili za maji, umeme, ulinzi na usafi…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kengele ya pili ilishagonga. Asante sana.

MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nauunga mkono hoja. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na afya njema. Si kwa ujanja wetu bali ni kwa huruma na rehema yake. Nitumie nafasi hii kuwashukuru sana wananchi wa Mkoa wa Singida kwa kumchagua Mheshimiwa Rais kwa kura nyingi za kishindo, Madiwani na Wabunge wa CCM. Nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia niwashukuru sana wapiga kura wangu wanawake wa Mkoa wa Singida ambao wamenipa fursa ya kuwawakilisha katika Bunge letu tukufu. Ninawashukuru sana ninakiri kwamba ninalo deni kubwa kwao la kuwawakilisha na pia kamwe sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikupongeze wewe kwa kuwa Spika wa viwango, mwenye kujali maslahi ya Wabunge wake na ambaye umeleta mapinduzi makubwa sana ya kidijitali katika Bunge letu. (Makofi)

Mheshimiaw Spika, ninaipongeza sana hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo imetoa dira na mwelekeo wapi Tanzania mpya tunatakiwa kuwa katika miaka mitano ijayo. Ni hotuba iliyogusa sekta zote muhimu katika kukuza uchumi, ni hotuba iliyogusa maslahi mapana ya wanyonge. Ni hotuba inayokwenda kutofautisha Tanzania na nchi nyingine za Afrika katika suala zima la kukuza uchumi. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiisoma hotuba hii ya Mheshimiwa Rais utatambua kwamba Mheshimiwa Rais anayo dhamira ya dhati ya kujenga Tanzania mpya ya kuifikisha uchumi wa juu kabisa. Ukurasa wa 10 wa kitabu cha Mheshimiwa Rais ameahidi kuongeza juhudi za kuwapa mikopo isiyo na riba au yenye riba nafuu. Pia ameagiza mifuko na programu mbalimbali ambazo zitasaidia uwezeshwaji wa wananchi kiuchumi kuunganishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili limewafurahisha sana wananchi na vijana wa Mkoa wa Singida na wameniagiza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa uamuzi huo na kwa kuwa asilimia 10 zinazotolewa katika Halmashauri zetu hazikidhi mahitaji ya wananchi wetu. Niiombe sana Serikali iharakishe mchakato wa kuunganisha mifuko hiyo ili wale bodaboda wangu, mama na baba lishe na wajasiriamali wadogo wadogo waweze kunufaika na mifuko hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia makundi haya utaona kwamba ni makundi ambayo hayana dhamana ya kukopa kwenye benki zetu, hivyo uwepo wa mfuko huo utawasaidia sana wananchi wale wa kipato cha chini kuweza kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali ya Awa,u ya Tano kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika utekelezaji wa miradi ya maji lakini nikiri kwamba bado kuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa maji safi na salama hususan maeneo ya vijijini. Mfano, katika mkoa wangu wa Singida upo mradi mkubwa wa Kitinku - Lusulile. Mradi huu umekuwa ukisuasua kwa muda mrefu bila ya kukamilika. Niiombe sana Serikali katika bajeti ya mwaka ujao itenge fedha za kutosha ili miradi ile ambayo haijakamilika ikiwemo huu Mradi wa Kitinku – Lusilile uweze kukamilika na wannachi waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na wenzangu katika suala zima la kilimo ambapo katika hotuba ya Mheshimiwa Rais...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Aysharose.

MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, ninaunga mkono hoja kwa asilimia 100. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na kutuwezesha kuuona mfungo huu wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza sana dada yangu Mheshimiwa Ummy kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuongoza Wizara hii ya TAMISEMI, lakini pia niwapongeze sana Manaibu, Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange pamoja na Mheshimiwa Silinde kwa kazi nzuri ambayo wameanza kuifanya. Nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali kwa kujikita katika ujenzi wa miundombinu ya shule za sekondari. Hata hivyo, nikiri kwamba shule hizi zina upungufu mkubwa sana wa walimu. Naiomba Serikali itazame Mkoa wangu wa Singida kwa jicho la kipekee, kwani Wilaya zangu za Mkalama, Singida DC, Iramba, Manyoni zina upungufu mkubwa sana wa walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile nangependa kujikita katika suala zima la afya katika Mkoa wangu wa Singida. Tunayo hospitali yetu nzuri ya Wilaya ya Manyoni, lakini hospitali hii ina changamoto kubwa sana ya majengo, majengo mengi ni finyu na pia ni chakavu kwasababu hospitali hii imejengwa muda mrefu sana, miaka ya 1950.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Halmashauri yetu ya Wilaya ya Manyoni imetenga eneo, naiomba sana Serikali katika bajeti hii iweze kutujengea hospitali mpya ya wilaya na vilevile kukarabati hospitali hii ambayo sasa ni chakavu na majengo yake ni finyu na hospitali hii ibaki kama Kituo cha Afya kwa kuwa kata yetu ya Manyoni haina Kituo cha Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba nichangie kuhusu hospitali yetu ya Wilaya ya Singida DC. Hospitali hii imekamilika lakini changamoto kubwa, jengo la wazazi halijakamilika. Naiomba sana Serikali ituwezeshe kutupa fedha ili jengo hili nalo liweze kukamilika na sasa wanawake na akina mama waweze kupata huduma bora za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunacho kituo chetu kizuri kabisa cha Mgori kimeshakamilika. Nakushukuru na wewe uliweza kukitembelea kituo hiki wakati wa kampeni, lakini kituo hiki hakina vifaa tiba. Naiomba sana Serikali pia itutazame kwa jicho la kipekee iweze kutupatia fedha kwa ajili ya vifaa tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee suala la uwezeshaji wa vikundi vya wanawake na vijana. Tunazo asilimia 10 zinatolewa katika halmashauri zetu, lakini nikiri kwamba asilimia hizi hazitoshi kukidhi mahitaji ya wananchi wetu. Ipo Mifuko ya Maendeleo ya Wanawake na Maendeleo ya Vijana. Naomba sasa Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na TAMISEMI washirikiane ili sasa wananchi waweze kuitambua mifuko hii na waweze kupata mikopo mingi zaidi kwani mahitaji ni makubwa sana. Naiomba Serikali itazame upya utoaji wa asilimia hizi 10 kwani wanatoa fedha, itakuwa ni jambo jema sana iwapo watatoa vifaa ili mikopo hii sasa iweze kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami niungane na wenzagu kabisa ambao wamesimama hapa na kuzungumiza suala la barabara za TARURA. Naiomba sana Serikali iweze kutenga fedha za kutosha ili sasa tuweze kuwa na miundombinu mizuri katika vijiji vyetu na katika kata zetu. Natambua kwamba Serikali imefanya kazi kubwa kwa kuunganisha wilaya na wilaya na mikoa na mikoa, lakini upande wa vijijini bado hali ni tete especially katika wilaya zangu zote za Mkoa wa Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie suala la mwisho la kuomba tuongezewe watumishi katika vituo vyetu vya afya pamoja na hospitali zetu za wilaya. Katika Mkoa wangu wa Singida kuna uhaba mkubwa sana wa watumishi wa Kada ya Afya. Namwomba sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu atuongezee watumishi wa kutosha ili wananchi wa Mkoa wa Singida waweze kupata matibabu kwa ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja na ninakushukuru kwa nafasi. (Makofi
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Kipekee nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na afya njema. Nitajielekeza moja kwa moja kuchangia mifuko ya hifadhi na muda ukitosha nitachangia Shilika la NIDA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika, mifuko ya hifadhi ya jamii imebeba maisha ya watanzania, wafanyakazi na wakulima kutokana na umuhimu wa mifuko hii. Lakini ripoti ya CAG imeonesha uwepo wa deni kubwa ambalo ni la muda mrefu. Tukiangalia taarifa ya Kamati ukurasa wa 28 & 29 napenda kunukuu. “Hoja kubwa ambayo imepewa msisitizo na CAG katika mifuko ya hifadhi ya jamii ni uwepo wa deni la muda mrefu ambalo mifuko inadai kwa Taasisi mbalimbali na hasa Serikali.” Deni hili limekuwa likikwamisha sana wastaafu kupata mafao yao kwa wakati. Na nikilitaja deni hili ambalo Shirika la NSSF linadai ni shilingi trilioni 1.1 ambalo hadi sasa limefikisha miaka 10 deni hili halijalipwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine tunailaumu mifuko hii hailipi mafao kwa wakati lakini inakuwa na mzigo mzito wa deni hili ambalo sasa inafanya kutowalipa wastaafu kwa wakati. Kwa upande mwingine wa Shirika letu la NHIF Serikali inadaiwa kiasi cha shilingi bilioni 209.7. Ningeishauri Serikali iweze kulipa fedha hizi kwani zinaharibu mizania ya hesabu na kufanya utendaji wa shirika kutokufanya kazi ka ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulichangia ni Shirika letu la NIDA. Nielezee kwa masikitiko makubwa sana. Upatikanaji wa vitambulisho vya NIDA umekuwa na usumbufu mkubwa na hasa kwa wananchi wangu wa Mkoa wa Singida na Kagera. Nikielezea tu mfano mdogo, Wilaya ya Manyoni ina halmashari mbili, halmashauri ya Itigi na Manyoni. Lakini kituo kinapofanyikia usajili wa vitambulisho hivi vya NIDA ni Wilaya ya Manyoni. Mwananchi kutoka Rungwa anatembea kilomita 200 kufuata kitambulisho cha NIDA ambapo sasa kituo cha kusajili kipo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni.

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Serikali iangalie uwezekano wa kupata vituo vingi vya kuweza kusajili vitambulisho hivi na wote tunatambua kwamba vitambulisho hivi vina umuhimu sana na vinamtambulisha mtanzania. Mfano tu, ukitaka kufungua akaunti, kusajili line, kufungua biashara au kupata mkopo ni lazima uwe na kitambulisho cha NIDA. Kwa hiyo, unaweza kuona kwamba, umuhimu mkubwa wa vitambulisho hivi.

Mheshimiwa Spika, taarifa ya Kamati ya PAC ukurasa 31 imeonesha ukaguzi uliofanywa na CAG kwa mwaka 2020/2021; na umebaini uwezo mdogo wa kuzalisha vitambulisho hivi. Pamoja na kununua mashine mbili mpya ambazo zilianza kufanya kazi Januari, 2021. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, NIDA inatakiwa kujitathmini je, inayo uwezo wa kutoa huduma kwa wananchi? Mpango kazi wa NIDA wa 2020/2021 uliitaka NIDA kuzalisha vitambulisho milioni 13.7 lakini hadi kufikia Juni, 2021 lengo hilo halikufikiwa. Ni vitambulisho milioni 3 tu ndivyo vilivyoweza kuzalishwa na kufanya jumla ya vitambulisho milioni 9.4 ambavyo vyote vilikuwa vimezalishwa. Unaweza kuona ni jinsi gani huduma hii inavyosuasua na jinsi wananchi wanavyotaabika kupata vitambulisho hivi.

Mheshimiwa Spika, niishauri Serikali, ihakikishe vitambulisho hivi vinapatikana kwa wakati. Lakini pia ripoti ya CAG imebaini kwamba mkandarasi hakulipwa madeni yake.

Mheshimiwa Spika, napenda kuunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama yetu mpendwa, mama msikivu na mwenye huruma Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa uongozi makini na uwazi wenye kujali maslahi ya wananchi, nampongeza sana.

Pia nampongeza sana Waziri wa Maji Mheshimiwa Juma Aweso, Naibu Waziri Engineer Maryprisca Mahundi na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha Watanzania wanapata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi na mafanikio yaliyopatika katika utekelezaji wa miradi ya maji katika mkoa wangu wa Singida bado kuna changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji safi na salama katika mkoa wangu wa Singida hususan maeneo ya vijijini na hii ni kwa sababu wananchi wengi wanatumia visima virefu na vifupi katika kupata maji kwa matumizi yao ya kila siku.

Mheshimiwa Spika, jiografia ya mkoa wa Singida ni kame hivyo ni lazima kuwa na chanzo cha uhakika wa maji ambacho kitawezesha wananchi wa mkoa wa Singida na viunga vyake kupata maji safi na salama wakati wote kwa uhakika, hivyo naiomba Serikali iangalie Mkoa wa Singida kwa jicho la kipekee katika suala zima la upatikanaji wa maji.

Mheshimiwa Spika, nipongeze sana mkakati wa Serikali wa kutoa maji kutoa chanzo cha Ziwa Victoria ambao kwa sasa maji hayo yamefika Wilaya yangu ya Iramba katika Mji wa Shelui, naishukuru Serikali na kuipongeza sana lakini niiombe Serikali iyafikishe maji hayo Makao Makuu ya Wilaya ya Iramba, Mji wa Kiomboi ambao una changamoto kubwa ya upatikanaji wa vyanzo vya maji endapo maji hayo yatafika Kiomboi itakuwa ni faraja kubwa kwa wananchi wa Vijiji vya Urughu, Mntenkente na Kizaga, lakini maji hayo pia yafike hadi Wilaya nyingine za Singida zikiwemo za Singida Vijijini, Mkalama, Ikungi, Singida Mjini na Manyoni ili ziweze kupata maji ya uhakika.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulichangia ni mradi wa visima ishirini kwa Wilaya ya Ikungi ambavyo kwa sasa vimekamilika lakini visima hivi havina miundombinu. Ombi langu kwa Wizara kwa kuwa visima hivi vimechimbwa kwenye vijiji na vijiji hivyo vina vitongoji ambavyo vipo mbali na sehemu kisima kilipochimbwa uwepo wa visima hivyo hautakuwa na maana endapo visima hivyo havitawekewa miundombinu.

Mheshimiwa Spika, pia nitumie nafasi hii kuwapongeza sana watendaji wa RUWASA ambao wamekuwa wakifanya kazi nzuri katika mkoa wangu wa Singida. Nawapongeza sana lakini pamoja na pongezi hizo RUWASA Mkoa wa Singida inakabiliwa na uhaba mkubwa wa watumishi, kuna uhaba wa watumishi 42 pamoja na vitendea kazi, magari yaliyopo katika Wilaya zangu zote ni mabovu, ni gari moja tu ambalo ni zima. Je, kutakuwepo vipi na ufanisi wa utekelezaji endapo vitendea kazi muhimu kama magari hakuna? Hakutakuwa na ufanisi.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali ituongezee wataalam na vitendea kazi vya kutosha ili kazi za utekelezaji wa miradi ya maji hususan maeneo ya pembezoni ufanyike kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya yangu ya Mkalama ipo miradi ambayo utekelezaji wake ulianza mwaka 2014 lakini miradi hii mpaka leo hii haijakamilika na miradi ambayo imetumia fedha nyingi za walipakodi. Miradi hii ni mradi wa Gumanga wa vijiji vitano, mradi wa maji wa Nyaha ambao umetumia shilingi milioni 900 lakini nao haujakamilika, hapa niishauri Serikali nikiamini Serikali yangu ni sikivu, iundwe kamati kutoka Wizarani ili kubaini ni kwa nini miradi hii mpaka sasa haijakamilika? Pia ili kubaini nini changamoto ya kutokukamilika kwa miradi hiyo wakati wananchi wanaendelea kuteseka kwa kukosa huduma ya maji?

Mheshimiwa Spika, naishukuru Serikali kwa kuendelea kutenga fedha katika Mradi wa Maji Kintinku - Lusilile wa vijiji kumi na moja na kwa kuwa mradi huu ni wa muda mrefu na wananchi wamesubiri kwa muda mrefu kupata huduma hii muhimu ya maji na kwa kuwa maeneo ya kata ya Kintinku, Maweni na Makutopora maji yake ni ya magadi na hayafai kabisa kwa matumizi ya binadamu na kwa kuwa wananchi hutembea zaidi ya kilometa tano kufuata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, niiombe na kushauri Serikali itenge fedha za kutosha katika mradi huo ili umalizike na wananchi wafurahie uwepo wa Serikali yao ya Awamu ya Sita ambayo ni sikivu sana!

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja iliyoko mezani. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenijalia uzima na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Nikupongeze wewe kwa kazi nzuri unayoifanya kwa kuliongoza vyema Bunge letu.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Juma Aweso, Naibu wake Mheshimiwa Maryprisca na watendaji wote wa Wizara ya Maji kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha maji yanapatikana katika maeneo yote. Nawapongeza sana, lakini pia nimpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri anayoifanya ya kumtua mama ndoo kichwani na kuhakikisha maji yanapatikana katika Mkoa wangu wa Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Singida, nampongeza sana na namshukuru sana. Maji ni uhai, pamoja na pongezi hizo, Mkoa wangu wa Singida bado una changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa maji safi na salama. Natambua jitihada kubwa za Serikali za kuhakikisha maeneo yote yanapata maji hususan ya vijijini lakini mkoa wangu bado una changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Serikali kwa Wilaya yangu ya Manyoni kupata maji katika Vijiji vya Rift Valley, Kintinku, Lusilile, Makasuku, Sasilo na uchimbaji wa maji visima 10 lakini upo mradi ambao tumekuwa tukiupigia sana kelele, Mradi wa Maji Kintinku, Lusilile. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kutupatia fedha kiasi cha bilioni tano. Niiombe sana Serikali, basi fedha hizi zitoke kwa wakati ili sasa mradi huu uweze kukamilika, kwa kuwa umekuwa ni wa muda mrefu toka Awamu ya Nne, mradi huu hadi sasa haujakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru pia Serikali kwa kupata miradi katika Wilaya yangu ya Mkalama ambapo ni Kijiji cha Singa, Tumuli, Mdilike, Matongo pamoja na uchimbaji wa visima 10, lakini yapo maeneo ambayo bado hayana maji kabisa katika Wilaya ya Mkalama. Maeneo haya ni Vijiji vya Mwangeza, Kisiluhida pamoja na Singa. Yana changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa maji, niiombe Serikali iviangalie kwa jicho la kipekee vijiji hivi ili navyo viweze kuapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru pia Serikali kuweka Mradi wa Maji Vijiji 28 na katika Mkoa wangu wa Singida tumeweza kupata Kiomboi, Manyoni pamoja na Singida Manispaa, lakini bado ipo miji ambayo inakuwa kwa kasi kama vile Ilongero, Ikungi, Mitundu na Nduguti. Niombe sana basi miji hii nayo iweze kupatiwa fedha kwa ajili ya upanuzi wa miradi ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya yangu ya Singida Vijijini, tumepata Mradi wa Semfuru, Ndugira, Ikiwu na Kinyamwenda, lakini kipo kijiji kimoja ambapo kupata chanzo cha maji ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo, niombe sana kijiji hiki cha Mangida nacho kiangalie kwa jicho la pekee. Yapo maeneo ya karibu ambayo yana ambapo maji hayo yanaweza kuvutwa hadi kupelekwa katika kijiji hicho cha Mangida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wangu wa Singida kuna changamoto kubwa ya watumishi na niombe pia Serikali iangalie na tuweze kupata watumishi wa kutosha katika Mkoa wangu wa Singida ili utekelezaji wa miradi ya maji uweze kufanyika kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze sana watendaji wa RUWASA katika Mkoa wangu wa Singida ambao wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana ya kuhakikisha maji yanapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache, naunga mkono hoja na nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Afya. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, Mwingi wa Neema kwa kunijalia afya na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Nimpongeze sana Waziri wa Afya, dada yangu Mheshimiwa Ummy, Naibu Wake, watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha Watanzania wanapata huduma bora za afya. Nawapongeza sana sana.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais mnyenyekevu, msikivu, Rais mwenye huruma na mapenzi makubwa kwa Watanzania. Hii imejidhihirisha wazi katika bajeti hii, tumeona namna ambavyo ameweza kuongeza fedha ili Watanzania waweze kupata huduma bora za afya. Mheshimiwa Rais tunakupongeza sana.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii, kwa niaba ya wananchi na wanawake wa Mkoa wa Singida kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa miradi mingi ambayo ametupatia katika Mkoa wangu wa Singida; miradi ya afya, vituo vya afya vimejengwa, Hospitali za Wilaya ya Mkalama, Ikungi pamoja na Hospitali ya Wilaya ya Ilongero ninampongeza sana Mheshimiwa Rais, tunamshukuru sana.

Mheshimiwa Spika, ningependa kugusia kuhusu Hospitali yangu ya Rufaa ya Mkoa wa Singida. Hospitali hii ujenzi wake umekuwa ni wa muda mrefu sana. Mheshimiwa Ummy, dada yangu amewahi kuitembelea hospitali hii pamoja na Mheshimiwa Dkt. Mollel na viongozi mbalimbali, lakini hospitali hii ya rufaa hadi sasa haijakamilika. Namwoamba sana Mheshimiwa Ummy hospitali hii ya rufaa sasa hivi ikamilike ili wananchi wa Mkoa wa Singida nao waweze kupata matibabu ya kibingwa katika Hospitali hii ya Rufaa ya Mkoa wa Singida.

Mheshimiwa Spika, hospitali hii ikikamilika itaweza kuwahudumia hata wananchi wa mkoa Jirani kama Tabora, Simiyu pamoja na Shinyanga. Naomba sana Serikali itenge fedha ili hospitali yetu hii ya rufaa iweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, pia hospitali zangu za Wilaya ya Singida hazina vifaa tiba vya kutosha na wataalamu. Naomba Serikali iweze kuleta wataalam pamoja na vifaa tiba ili sasa matibabu yaweze kutolewa kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, Hospitali yangu ya Wilaya ya Mkalama, Ikungi pamoja na Manyoni zina changamoto kubwa ya watumishi. Naomba mtuletee watumishi. Mkalama ina ukosefu wa watumishi 750, Ikungi ina ukosefu wa watumishi 1,022 na Manyoni kuna ukosefu wa watumishi 350.

Mheshimiwa Spika, kama Wabunge wenzangu walivyotangulia kusema, kwamba uwepo wa majengo mazuri, yanatakiwa pia yawe na vifaa tiba pamoja na watumishi. Pia vipo vituo vya afya, ambavyo ni Sepuka, Mgori, pamoja Msange, havina magari ya kubebea wagonjwa na pia havifanyi upasuaji. Naomba sana vituo hivi vya afya viweze kupata vifaa tiba pamoja na magari ya kubebea wagonjwa ili huduma bora za afya kwa mama na mtoto ziweze kutolewa.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa haya machache, naunga mkono hoja na ninaendelea kuwapongeza sana madaktari wote na wauguzi wote kwa kazi nzuri ambazo wameendelea kuzifanya, ni kazi ya thawabu, Mwenyezi Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja hii muhimu kwa mustakabali wa makundi maalum ya wanawake.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Dkt. Dorothy Gwajima, Naibu wake, Mheshimiwa Mwanaidi Katibu Mkuu, Dkt. Jingu pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais ambaye amekuwa mstari wa mbele kuyajali makudi maalum, lakini pia kwa namna ambavyo ameendelea kuwatumikia Watanzania kwa moyo wa upendo, nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nitumie nafasi hii kukupongeza wewe binafsi kwa kazi nzuri ambayo unaifanya na namna ambavyo unaliendesha Bunge letu, nakupongeza sana. Paada ya pongezi hizo, nijielekeze moja kwa moja kwenye mchango wangu. Kila kukicha tunasikia vitendo vya ukatli vikishamiri katika jamii. Unasikia mtoto amebakwa huku, unasikia mtoto kalawitiwa kule, unasikia mwanafunzi ametoroshwa, unasikia mwanamke amepigwa, vitendo hivi vimezidi kushamiri katika jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe sana jamii yangu iweze kubadilisha mtazamo wa masuala haya, pia niiombe Serikali iweze kuangalia kwa kina na kuja na mkakati mahsusi wa mafunzo maalum kwa ajili ya jamii katika ngazi zote kuanzia Kata, Vijiji hadi Vitongoji. Wahakikishe kabisa mafunzo haya yanafika,kwa sababu vitendo hivi vya ukatili wa kijinsia vinatokea katika ngazi ya familia. Utasikia mjomba leo amembaka mtoto wa dada yake, baba mdogo kambaka mtoto wa shemeji yake. Kwa hiyo ni muhimu sana mafunzo yakafanyika katika ngazi zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze sana Serikali, pamoja na mikakati mbalimbali ambayo wanaifanya kwa kila siku ya kuelimisha jamii, lakini bado nguvu kubwa inatakiwa kuwaelimisha jamii ili sasa waweze kuepukana na vitendo hivyo.

Mheshimiwa Spika, pia naomba sana sasa kuwepo na haya madawati ya ukatili wa kijinsia katika kila sehemu, kuanzia ngazi ya kata na ngazi ya Kijiji ili yaweze kutoa miongozo mbalimbali na kuwasaidia wananchi kuweza kuepukana na vitendo hivi vya ukatili wa kijinsia.

Mheshimiwa Spika, vile vile katika Mkoa wangu wa Singida kuna changamoto kubwa ya uhaba wa watumishi wa kada ya Maafisa Maendeleo ya Jamii. Hawa ndio wanaobadilisha mitazamo katika jamii, na ndio wanaoisaidia jamii kubadilisha uelekeo wa maisha yao. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali iajiri Maafisa Maendeleo ya Jamii wa kutosha ili sasa kazi nzuri za Maafisa Maendeleo ya Jamii ziweze kufanyika katika kila eneo na katika kila sehemu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la mikopo. Naipongeza sana Serikali ambayo imeendelea kutoa mikopo kwa makundi maalum ya wanawake, vijana na wenye ulemavu. Natambua kwamba kwa sasa wamesitisha, kwa hiyo, naomba wafanye maboresho haraka ili mikopo hii iweze kutoka kwa makundi haya ya vijana, wanawake na wenye ulemavu, kwa sababu imekuwa ni mkombozi mkubwa sana kwa wao kujikwamua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa haya machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi na mimi niweze kutoa mchango katka Wizara hii ya Nishati na awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mungu kwa baraka na neema zake na kwa kunijalia uzima na afya njema. Niungane na Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake imara na kazi nzuri anayoendelea kuifanya ya kuleta mabadiliko makubwa katika Taifa letu. Nitumie nafasi hii kumpongeza sana Waziri wa Nishati Mheshimiwa January Makamba, Naibu wake Mheshimiwa Stephen Byabato na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri na kubwa ya kuhakikisha nchi yetu inapata nishati ya kutosha, hongereni sana! Napenda kuwatia moyo endeleeni kuchapa kazi na sisi tupo nyuma yenu.

Mheshimiwa Spika, nitachangia maeneo yafuatayo; nianze na Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, niipongeze sana Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi imara wa Jemedari Mheshimiwa Rais Daktari Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa za kuendelea kutekeleza mradi huu kwa weledi mkubwa na kuhakikisha unakamilika kwa malengo waliyojiwekea.

Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameonesha nia ya Serikali ya kukamilisha mradi kwa sasa mradi huu umefikia 87%; ni jambo kubwa na la kujivunia uzinduzi wa kujaza maji kwenye mradi huu wa Bwawa la Mwalimu Nyerere uliofanywa na Mheshimiwa Rais unatoa dira kama nchi tumeamua kuondokana na giza na kukaribisha mwanga kuliwezesha Taifa letu kupata nishati ya kutosha kwa kuwa mradi huu umegharimu fedha nyingi. Niishauri Serikali iongeze kasi ya utekelezaji wa mradi huu ili thamani ya fedha iweze kuonekana. Ninaamini kumalizika kwa mradi huu utakuwa ni kichocheo kikubwa cha kuleta maendeleo na kutavutia wawekezaji wa kutoka ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo ningependa kulichangia ni mradi wa REA; niipongeze sana Serikali kwa kuendelea kusambaza umeme kuhakikisha umeme unafika kila pembe ya nchi yetu vijijini, lakini bado jitihada kubwa zinatakiwa kufanyika ili vijiji vyote na vitongoji vyote viweze kupata nishati ya umeme. Katika mkoa wangu wa Singida kuna vijiji 441 kati ya vijiji hivyo vijiji 114 havijawashwa umeme, Ikungi vijiji 24, Iramba vijiji 10, Wilaya ya Manyoni vijiji 26, na Wilaya ya Singida 18. Niiombe Serikali iharakishe na vijiji hivi viweze kupata nishati ya umeme kwa haraka na wa kati.

Mheshimiwa Spika, niungane na Wabunge wenzangu pamoja na kwamba umeme umefika vijijini lakini bado vitongoji vingi havijafikiwa, niishauri Serikali ije na mpango mkakati wa kuhakikisha vijiji na vitongoji vyangu vyote vya mkoa wa Singida vinapata umeme, lakini pia Serikali iangalie upya bei za umeme hususan maeneo ya Miji Midogo kwani miji yangu ya Iguguno, Nduguti, Ikungi, Ilongero na Kiomboi hali zao ni za chini na hawana uwezo wa kulipa gharama ya shilingi 320,000 ili malengo mazuri yaliyowekwa na Serikali yaweze kutimia.

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho ambalo ningependa kulichangia ni matumizi ya gesi majumbani yaani nishati safi majumbani, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa maono makubwa ya ustawi wa jamii hususan kwa kundi la wanawake kwani ndio wahusika wanaotumia gesi hii majumbani, kwa sasa ni asilimia ndogo sana ya Watanzania wanaotumia nishati safi kwa kupikia yaani gesi, niiombe Serikali ije na kampeni kubwa ya kuelimisha jamii juu ya matumizi ya nishati safi ya gesi majumbani ili wananchi wetu wengi waweze kuachana na nishati chafu ambayo kwa kiwango kikubwa imeharibu mazingira na vyanzo vya maji na ningependa kushauri kampeni hii iitwe “Achia Shoka, Kamati Gesi,” lakini niiombe sana Serikali ili maono makubwa ya Mheshimiwa Rais yaweze kutimia ni lazima gesi ipatikane kila mahala kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza watendaji wote wa TANESCO na REA wakiongozwa na Engineer Florence Godfrey Mwakasege Meneja wa Mkoa wangu wa Singida kwa kazi nzuri na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na neema kwa kutujalia uzima. Nikupongeze wewe kwa usimamizi na uendeshaji mzuri wa Bunge letu tukufu. Kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake imara na dhamira yake ya dhati ya kuleta mabadiliko makubwa katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Waziri wa Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Mohammed Mchengerwa, Naibu wake Dada yangu, Mary Masanja na timu yao kwa kazi kubwa na nzuri wanaoiyafanya kwenye Wizara hii. Hii ni miongoni mwa Wizara muhimu kwenye uchumi na ukuaji wa uchumi wetu. Kama Taifa linaloendelea, tunahitaji kuwa na sekta imara ya utalii na ninyi ni watu sahihi kwa sababu mnaifanya kazi hiyo kwa weledi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, sikuweza kupata nafasi ya kusimama kuchangia, lakini naomba nifikishe mawazo yangu kwa maandishi ili kusaidiana na kaka yangu Mchengerwa na dada yangu Mary kueleza mambo machache.

Mheshimiwa Spika, nianze na utalii; nipongeze jitihada kubwa zinazofanyika katika kuvutia watalii nchini. Kwa takwimu za Wizara ni kwamba zaidi ya watalii milioni 1.4 wametembelea hifadhi na mbuga zetu za wanyama. Haya ni mafanikio makubwa sana, lakini nadhani bado tuna kazi kubwa ya kufanya ili kuongeza tija zaidi. Natambua yapo maeneo mengi ambayo kama tutaweka mkakati wa kuyafikia basi tunaweza kuwa na idadi kubwa zaidi ya tuliyonayo sasa. Kwa mfano, Mkoani kwangu Singida tuna ardhi nzuri na hali ya hewa rafiki kwa watalii, uwepo wa Ziwa Singidani lenye ndege adimu, lakini nyumba za utamaduni (tembe, vibuyu na vipeyu). Hili ni eneo ambalo linaweza kuongeza tija kwa watalii kwa kuwa sio kila mtalii anakuja nchini kuangalia wanyama, wengine hufuata kujifunza tamaduni, mbali na hilo Singida ni mkoa ambao uko katikati ya nchi hivyo kutangazia dunia kuwa ukiwa hapa ndio utakuwa katikati kabisa mwa Tanzania kila mtalii atatamani kuona Singida inafanana vipi.

Mheshimiwa Spika, ikumbukwe kuwa Singida kuna mlango wa mkondo wa bonde la ufa katika Kijiji cha Kinyamwenda, lakini bado hakuna jitihada za makusudi kulihifadhi eneo hilo ama kulitangaza kwa nguvu katika kuvutia utalii.

Kuhusu mapori ya akiba; mkoani kwangu kuna mapori ya akiba ya Mgori na Rungwa ambayo ni muhimu kwa ustawi wa Taifa letu. Mapori haya ni sifa na fahari kwa wananchi wa Singida. Lakini kuna mambo ambayo kama Serikali tunapaswa kuyapa kipaumbele. Wanawake wa Singida bado ni masikini hivyo, naomba uwepo wa mapori haya ukawe na baraka kwao. Wengi walikuwa wakihemea kuni kwenye maeneo ya jirani nje ya mapori, lakini kwa sasa wanakutana na vitendo viovu. Itoshe kusema basi ukatili huu dhidi ya wanawake ukomeshwe na Wizara ione umuhimu wa kusaidiana na jamii kwa kuwapa wanawake hawa majiko ya gesi ili wawe mabalozi wazuri wa kulinda mazingira ya ndani na nje ya mapori haya. Kwenye maeneo mengine yanayohusika na Hifadhi za Taifa kama Ngorongoro, mamlaka imekuwa mstari wa mbele kushirikiana na jamii kupitia CSR, basi na huku ikawe hivyo.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ningependa kulichangia ni kuomba Wizara ya Maliasili na Utalii itenganishwe kuwe na Wizara ya Utalii na kuwe na Wizara ya Maliasili na Mambo ya Kale. Kwa nini nasema hivyo Wizara ya Maliasili na Utalii imekuwa ikitumia muda mwingi kushughulikia migogoro ambayo inatokea kwenye mapori ya hifadhi badala ya kutumia muda huo kutafuta namna bora ya kutangaza vivutio vyetu na kuutangaza utalii wetu ambao una vivutio vingi ambavyo bado hatujavitangaza vizuri.

Mheshimiwa Spika, nawasilisha na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii muhimu ya kilomo. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima na afya njema. Nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuijenga nchi yetu na kwa namna ambavyo ametoa kipaumbele kikubwa katika bajeti hii ya kilimo. Nampongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugawaji wa pikipiki elfu 700, vishikwambi, 384 na extension kits 6,700 ni kilelezo tosha Mheshimiwa Rais anayo dhamira ya dhati ya kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya kilimo. Niwaombe sana Watanzania tumuombee mama yetu mpendwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ili aweze kuendeleza nchi yetu na aweze kuongoza vyema Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Bashe Naibu wake Antony Mavunde, Katibu Mkuu Edward Massawe na watendaji wote wa Wizara hii ya Kilimo kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya ya kuhakikisha kilimo chetu kinakuwa ni kilimo chenye tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia katika eneo la umwangiliaji na endapo muda utatosha nitachangia katika zao la alizeti na zao kitunguu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana mabadiliko ya tabia nchi na mazingira yetu jinsi yalivyobadilika tunahitaji kujikita katika kilimo cha umwangiliaji na si kilimo cha kutegemea mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wangu wa Singida ni miongoni mwa mikoa ambayo ni mikoa yenye jiografia iliyo kame sana. Hivyo, tunahitaji sana kuwekewa mabwawa ya umwangiliaji ili kuweza kuendeleza kilimo kwa msimu wa muda wote. Ninaomba sana tuweze kujengewa mabwawa ya kutosha katika Mkoa wetu wa Singida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulichangia ni kuhusu Skimu ya Umwangiliaji ya Mbwasa. Niishukuru sana Serikali imeweza kututengea fedha katika bajeti hii kwa ajili ya kuendeleza skimu hii ya Mbwasa. Hata hivyo, kwa kuwa usanifu yakinifu umeshafanyika naupembuzi niombe sasa skimu hii ianze kufanya kazi na utekelezaji wa skimu hii uanze mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunalo Bwawa Mngamo pamoja na Bwawa la Msange ambapo wananchi wa eneo hilo wanatumia maji hayo kwa ajili ya kuendeleza shughuli za Kilimo. Niiombe Serikali, endapo mabwawa haya yataendelezwa yataweza kuwa na tija sana kwa wananchi wa Mkoa wangu wa Singida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Bashe alikuja akayatembelea Mabwawa haya ya Mngamo Pamoja na Msange na kujionea namna ambavyo mabwawa haya yanavyowanufaisha wananchi wa eneo hilo. Sasa nikuombe, kwa kuwa ulishatuma wataalam wakuja kuweka michoro na michoro hiyo imeshakamilika niombe sana sasa kazi hii iweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wangu wa Singida tunalima zao la alizeti na kitunguu. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye amekuwa ni kinara katika kuendeleza zao hili la alizeti. Pia nipongeze sana Serikali ambayo ilitoa mbegu kupitia taasisi yetu ya ASA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini yako maeneo mengine mbegu hizi zimezalisha alizeti vizuri lakini maeneo mengine mbegu hizi azijazalisha alizeti vizuri. Hivyo niiombe taasisi hii iendelee kufanya utafiti ili sasa kwa msimu unaokuja maeneo yote yaweze kulima alizeti na tuweze kuzalisha zaidi alizeti katika Mkoa wangu wa Singida, na vile vile ili upungufu wa mafuta uwe ni historia katika nchi yetu katika Mkoa wa Singida…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na ninaunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu kwa ajili ya maendeleo ya wanawake. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazozifanya na kuona umuhimu wa kuwa na Wizara hii ya wanawake na makundi maalum ambayo uwepo wake imesaidia sana kutatua kero na changamoto za wanawake ambao ndiyo walezi wa familia na jamii kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, dada yangu Dorothy Gwajima, Naibu wake Mwanaidi Ali, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya kuhakikisha wanatatua changamoto za makundi maalum, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo napenda kulichangia ni Maafisa Maendeleo Jamii na uwezeshwaji wa wanawake kiuchumi; Maafisa Maendeleo Jamii ni watu muhimu sana katika jamii na napenda niseme kwamba ni changes agency ambao wanabadilisha mindsets katika jamii, lakini wamekuwa wakisahaulika sana, Serikali imekuwa haiwapi kipaumbele. Wamekuwa wakifanya kazi kwenye mazingira ambayo siyo rafiki, lakini pia hawana vitendea kazi na nyenzo nyingine muhimu za kuwasaidia kufanikisha majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni kumekuwepo na matukio mbalimbali ya ubakaji kwa watoto wa kike lakini pia ulawiti kwa watoto wa kiume na vitendo vingine ambavyo kwa kweli havipendezi sana katika jamii yetu. Endapo viongozi hawa, Maafisa Maendeleo Jamii hawa wangeweza kuwezeshwa vizuri vitendea kazi na nyenzo nyingine muhimu kama ambavyo Maafisa Ugani wameweza kuwezeshwa pikipiki na vitendea kazi vingine wangeweza kufanya kazi kwa ufanisi na kuweza kuyafikia makundi mengi sana katika jamii, kuwapa elimu juu ya lishe bora, malezi bora lakini pia kuwapa elimu juu ya jambo hili muhimu ambalo liko mbele yetu sensa na makazi ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niishauri Serikali iwaangalie sana Maafisa Maendeleo Jamii hawa, kama wenzangu walivyotangulia kusema ni watu ambao wanagusa karibia kila sekta, wakiwezeshwa wataweza kuyafikia makundi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, lakini pia katika Mkoa wangu wa Singida kuna uhaba mkubwa sana wa Maafisa Maendeleo Jamii hususan katika Kata, wale Maafisa Maendeleo Jamii ambao wako Wilayani kutokana na jiografia ya Mkoa wa Singida hawawezi kufika kila sehemu. Maeneo ambayo wanaweza kufika ni maeneo machache sana. Lakini endapo kutakuwa na Maafisa Maendeleo ya Jamii katika kila kata wataweza kuielimisha jamii na vitendo hivi mfano vya ukatili wa kijinsia ukiwepo wa kubaka watoto, ulawiti wa watoto wa kiume, mmomonyoko wa maadili, wataweza kuielimisha jamii na mambo hayo yataweza kupungua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo napenda kulichangia ni uwezeshwaji wa wanawake kiuchumi; ni ukweli usiopingika, ukimwezesha mwanamke umeiwezesha jamii. Lakini ipo mikopo ambayo inatolewa katika halmashauri, mikopo ya asilimia 10; wenzangu wametangulia kusema, mikopo hii haitoshi kabisa, lakini pia imekuwa ni mikopo ambayo haina tija. Mfano kikundi kina watu 15, wanapewa kiasi cha shilingi milioni tatu, wanaishia kugawana laki mbili, mbili. Hapo tija iko wapi? hakuna tija yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikari ni vyema sasa kuiangalia na kuitathimini mikopo hii na kuangalia njia bora zaidi za kuweza angalau kuwapa mradi. Mfano mradi wa kufuga kuku au mradi wa kulima mbogamboga au mradi hata wa kufuga nyuki pamoja na kuwapa mafunzo. Jambo hili lingekuwa linatija sana kwa wanawake ambao hawa wanawake ndiyo walezi wa jamii na walezi wa familia lakini wamekuwa wakiangalia matibabu, wamekuwa wakilipa hata ada za watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napenda kuishauri Serikali ni vizuri sasa kukawepo mkakati mahususi wa kuangalia namna bora zaidi, kwa sababu nimejaribu kuangalia hapa kwenye bajeti, lakini sijaona mahali popote ambapo kuna mkakati mahususi wa kupinga hivi vitendo vya ukatili wa kijinsia hususani ubakaji wa watoto wa kike ambao wamekuwa watoto innocent, hawana hatia, hawajui, wanakuwa wanaharibika kisaikolojia. Naishauri sana Serikali kuweko na mkakati wa kitaifa wa kuweza kuendesha kampeni ya kuzuia ukatili wa kijinsia.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja na nawapongeza sana viongozi wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya na nakupongeza wewe kwa kuliendesha Bunge letu vizuri. Nakushukuru. (Makofi)