Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Asha Mshimba Jecha (5 total)

MHE. ASHA MSHIMBA JECHA aliuliza:-
Kituo cha Polisi Dunga kimechakaa sana kwani kuta zake zimepasuka na baadhi ya vyumba havitumiki kutokana na kuhatarisha usalama wa askari na wananchi wanaofika kwa ajili ya kupata huduma. Je, ni lini Serikali itajenga upya kituo hicho?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na Kituo cha Polisi Dunga pamoja na Wilaya zote mpya zilizoanzishwa katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Kwa kutambua umuhimu wa Kituo cha Polisi Dunga, tathmini itafanyika ili gharama halisi ziweze kujulikana. Aidha, ujenzi wa kituo hicho utaanza mara baada ya fedha kupatikana kwa ajili ya kipaumbele cha Serikali na hivi sasa katika kukamilisha miradi ya zamani ya polisi na kuanza miradi mipya ya ujenzi wa vituo hivyo vya polisi.
Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za Serikali kuimarisha miundombinu ya ulinzi na usalama, tunatoa wito kwa wadau mbalimbali wa maendeleo kushiriki katika ujenzi wa vituo vya polisi ili huduma za ulinzi na usalma ziweze kupatikana kwa karibu.
ASHA MSHIMBA JECHA aliuliza:-
Mradi wa Kuwawezesha Wananchi Kiuchumi Vijijini (MIVARF) katika Mkoa wetu wa Kusini Unguja umeweza kuwakomboa wananchi kwa kuongeza uzalishaji wa mazao na kuboresha mawasiliano ya barabara na kuweza kusafirisha mazao yao kwa urahisi. Kwa kuwa mradi huu umeonesha mafanikio na wananchi wamehamasika.
Je, Serikali ipo tayari kuwaongezea mitaji na mafunzo wananchi hao ili waweze kufikia malengo yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. ANTONY P. MAVUNDE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha inaunga mkono juhudi za wananchi kushiriki katika uchumi wa kilimo kwa kusaidia upatikanaji wa mitaji na kuwapatia mafunzo stahiki. Hatua za kuwawezesha wananchi wa Zanzibar kimtaji zilianza kwa kuvijengea uwezo wa kiutawala na kiutendaji Vyama vya Kuweka na Kukopa (SACCOS) na vikundi vingine vya uzalishaji ili viweze kuratibu na kusimamia kwa ufanisi matumizi ya mitaji itakayopatikana kupitia mikopo inayotolewa na taasisi za kifedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, matayarisho yanaendelea ili kuvipatia vikundi vya wazalishaji ambavyo tayari vimehakikiwa na uwezo wao baada ya ziara ya uongozi wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kutembelea Zanzibar mwezi Mei, 2017. Benki hii ni mshiriki mkubwa wa MIVARF, ambayo huendesha mfuko wa dahamana (Guarantee Fund) wa mikopo utakaofanya benki kuwakopesha wakulima kwa masharti nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekit, tayari Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango na Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) wamesaini makubaliano ya uendeshaji wa mfuko wa dhamana tarehe 3 Novemba, mwaka 2017. Kwa kupitia makubaliano hayo, Serikali tayari imetoa shilingi bilioni 22 kwa TADB ili kuanza utekelezaji kwa kushirikisha benki za biashara kufikisha huduma ya mikopo kwa makundi mbalimbali. TADB walishaanza utaratibu huu kwa kutangaza kwenye magazeti ili kupata benki zitakazoshiriki. Nawashauri wananchi wote watumie fursa hii adhimu kujipatia mikopo ili kupanua shughuli zao za maendeleo na kujiongezea kipato. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa kitoa mafunzo mbalimbali kwa wananchi kupitia mradi wa MIVARF ili waweze kuyafikia masoko yenye tija. Mafunzo hayo ni pamoja mbinu bora za kilimo (good agricultural practice), uongezaji thamani mazao na jinsi ya kuyafikisha masoko yenye tija na kukuza na uimarishaji Vikundi vya Akiba na Mikopo (SACCOS). Programu kupitia kwa watoa huduma (Business Coaches) inaendelea kutoa mafunzo haya kwa wananchi hasa katika Nyanja za kuongeza thamani mazao na kuyafikisha masoko.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA aliuliza:-
Je, nini chanzo cha ugonjwa wa Lupa na ni watu wangapi wameugua na wangapi wamefariki kutokana na ugonjwa huo hapa Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ugonjwa wa Lupa au kwa jina la kigeni unajulikana kama Systematic Lupus Erythematosisni ugonjwa wa kinga za mwili ambao hushambulia viungo vya mwili vikidhania kwamba ni vitu vigeni (foreign bodies). Viongo ambavyo hudhurika zaidi ni ngozi, figo, ubongo, chembechembe za damu, moyo, mapafu na viungo vingine vya mwili kama joints. Watafiti hadi sasa hawajaweza kubaini chanzo cha ugonjwa huu. Inasadikiwa kwamba mgonjwa mwenye vinasaba vya Lupa hupata ugonjwa huu pale anapokutana na visababishi kwenye mazingira vinavyochochea kuanza kwa ugonjwa huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vitu vinavyoweza kuchangia kuanza kwa ugonjwa huu ni miale ya jua, maambukizi ya bakteria, matumizi ya baadhi ya dawa za shinikizo la damu, dawa za kifafa na antibiotic. Wagonjwa wenye ugonjwa wa Lupa unaotokana na dawa hupona haraka mara wanapoacha kutumia dawa hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, visababishi vingine vinavyoongeza uwezekano wa kupata ugonjwa huu wa Lupa ni pamoja na jinsia. Ugonjwa huu huwapata zaidi wanawake kuliko wanaume. Katika masuala ya umri, Lupa huwapata zaidi watu wenye umri kati ya miaka 15 hadi 45. Asili, Lupa huwapata zaidi Wamarekani wenye asili ya Kiafrika, Wahispania na Waasia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, dalili za ugonjwa huu siyo rahisi kubainika kirahisi. Baadhi ya dalili kuu ni maumivu ya viungo, uchovu wa mara kwa mara, homa, vidonda vya mdomoni na vipele vinavyofanana na mabawa ya kipepeo kwenye mashavu. Ugonjwa huu hauna tiba, dawa zinazotolewa hulenga kupunguza athari za ugonjwa tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili takribani wagonjwa wawili hugundulika na ugonjwa wa Lupa kwa mwaka na hufuatiliwa katika Kliniki ya Ngozi. Mpaka hivi sasa kuna wagonjwa takribani 10 wanaofuatiliwa katika hospital hii. Katika mwaka 2017/2018 kumeripotiwa kifo kimoja kutokana na ugonjwa huu. Kuna uwezekano wa vifo vingi zaidi kutokana na ugonjwa huu, lakini havijaripotiwa kutokana na dalili za ugonjwa huu kutobainika kirahisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba nimalizie kwa kusema kuwa ugunduzi wa ugonjwa wa Lupa ni mgumu sana na wakati mwingine mtu hutibiwa kama mgonjwa wa ngozi tu. Ni kutokana na ugumu uliopo wa kugundua na hata mtu kujua kama na ugonjwa wa Lupa, wagonjwa wengi hufika katika Hospitali wakiwa na matatizo mengine kama ya ngozi, viungo na hutibiwa matatizo waliokuja nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwa wananchi kujenga tabia ya kupima afya zao mara kwa mara ili kugundua kitu chochote kisichokuwa cha kawaida katika miili ili waweze kupata tiba mapema kabla tatizo halijawa kubwa zaidi.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA aliuliza:-

Tanzania imebarikiwa kuwa na Ukanda wa Bahari na Maziwa.

Je, wananchi wa maeneo hayo wameandaliwaje kufaidika na rasilimali zinazopatikana katika Ukanda wa Bahari na Maziwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sekta ya uvuvi nchini inasimiwa na sera, sheria pamoja na miongozo mbalimbali iliyoandaliwa kwa lengo la kuhakikishwa wananchi na Taifa linanufaika na rasilimali za uvuvi. Pia Sera ya Uvuvi inaelekeza ushirikishwaji wa wananchi katika kusimamia rasilimali za uvuvi ambapo vimeanzishwa vikundi vya usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi kwa maana ya BMU. Vikundi hivi vinalenga kuwawezesha wananchi katika maeneo vilipoanzishwa kuwa wanufaikaji wa kwanza wa rasilimali hizi kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali ya uvuvi endelevu.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanzisha Wakala wa Mafunzo ya Uvuvi ili kuwapatia elimu vijana wa Kitanzania kuhusu masuala ya uvuvi ili nchi inufaike na rasilimali za uvuvi tulizojaliwa. Pia, Serikali imeanzisha Taasisi ya Utafiti yaani TAFIRI ili kufanya tafiti na kuvumbua teknolojia zitakazosaidia kuleta tija kwenye tasnia ya uvuvi. Taasisi hizi husaidia kuwapatia elimu na maarifa wadau wa uvuvi.

Mheshimiwa Spika, vilevile Wizara ina mikakati mbalimbali inayolenga kuleta maendeleo katika sekta ya uvuvi na kuwasaidia wavuvi ambayo ni pamoja na:-

(i) Kuendelea kutoa elimu kwa wavuvi na wadau wote kuhusu uvuvi endelevu, sera, sheria na kanuni za uvuvi ili kulinda, kusimamia, kuhifadhi na kuendeleza rasilimali za uvuvi nchini kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo;

(ii) Kuwekeza katika uvuvi wa bahari kuu kwa kufufua Shirika la Uvuvi (TAFICO), kujenga bandari ya uvuvi, kununua meli mbili kubwa za uvuvi ili kuchochea ukuaji wa viwanda vya kuchakata samaki, kuongeza thamani ya mazao, ajira na kuongeza mapato ya Serikali; na

(iii) Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wavuvi kuhusu ukuzaji wa viumbe katika maji yaani aquaculture na ufugaji samaki kwenye vizimba kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa samaki kwenye maziwa na baharini.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeanzisha Dawati la Sekta Binafsi ili kuwasaidia wavuvi kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo kupata mikopo kutoka kwenye taasisi za fedha.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA aliuliza:-

Azma ya Serikali ya kuwafikishia wananchi huduma popote walipo ni njema. Aidha, naipongeza Serikali kwa ujenzi wa Kituo kipya cha Polisi Dunga baada ya jengo la awali kuwa bovu na kuvunjwa.

(a) Je, ni lini jengo hilo jipya litakamilishwa kwa kufanyiwa matengenezo yaliyobaki?

(b) Je, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi iko tayari kukipatia Kituo cha Polisi Dunga gari la huduma?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Kituo cha Polisi Dunga Daraja C ulianza mwezi Julai, 2018 na ulisimama mwezi Novemba, 2018 ukiwa umefikia hatua ya umaliziaji (finishing) ambayo tathmini yake inakadiriwa kufikia shilingi 49,862,220.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi linategemea kupata fedha hizo kutoka katika Mfuko wa tuzo na tozo na zitatumiwa katika mfumo wa nguvu kazi (Force Account).

(b) Mheshimiwa Spika, Kituo cha Polisi Dunga kipo katika Wilaya ya kati Mkoa wa Kusini Unguja. Mkoa mzima una jumla ya magari ya Polisi 17. Wilaya ya kati peke yake ina magari mawili mazima. Jeshi la Polisi limekuwa likigawa magari kwa awamu kwa kadiri yanavyopatikana. Kituo cha Polisi Dunga ni miongoni mwa vituo vitakavyopatiwa magari pindi yatakapopatikana.