Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Anastazia James Wambura (19 total)

MHE. KHATIBU SAID HAJI aliuliza:- Mheshimiwa Spika, Sheria za FIFA zimekataza mambo yanayohusiana na mchezo wa soka kupelekwa Mahakamani:-
(a) Je, Serikali inatoa tamko gani juu ya makosa yanayofanyika katika klabu za soka?
(b) Je, ni kwa kiasi gani sheria hizi za FIFA zinakinzana na Sheria za nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mbunge wa Konde, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Sheria za FIFA zinakataza mambo yanayohusiana na soka kupelekwa Mahakamani. Hatua hiyo inalenga kuwezesha masuala yote yanayohusiana na soka kuendeshwa kwa kufuata na kuzingatia taratibu na miongozo iliyowekwa na mamlaka za mchezo huo katika ngazi mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, aidha, hatua hiyo imewezesha mchezo wa soka kuchezwa na kupata matokeo kwa wakati na hivyo kuepusha mazuio ya Mahakama ambayo yanaweza kusababisha usumbufu usio wa lazima kwa washiriki wengine.
Mheshimiwa Spika, utaratibu huo unazifanya mamlaka mbalimbali zinazosimamia mchezo huo kuwa na Katiba zinazowawezesha kupokea, kusikiliza na kutoa uamuzi dhidi ya malalamiko, rufaa na kero za wadau wa klabu au chama cha soka husika.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatoa wito kwa vyama, vilabu na mashirikisho ya mpira wa miguu kuzingatia na kufuata taratibu zilizowekwa kwa mujibu wa Katiba zao ili kupunguza migogoro inayoweza kujitokeza katika uendeshaji na uendelezaji wa soka nchini.
(b) Mheshimiwa Spika, maendeleo ya michezo hapa nchini yanaendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Baraza la Michezo ya mwaka 1967, kama ilivyorekebishwa na Sheria Na. 6 ya mwaka 1971. Sheria hii ni kongwe na ina baadhi ya mambo ambayo yanakinzana na Sheria za FIFA. Serikali inafanya mapitio ya sheria hiyo ili iendane na wakati kwa lengo la kuboresha na kuendeleza michezo nchini.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma unaongoza kwa kuwa na vijana wengi wanamichezo na wasanii mfano Shaaban Robert, Diamond, Ali Kiba, Banana Zoro, Linex, Mrisho Mpoto na kadhalika:-
(a) Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika Mkoa wa Kigoma kwa kujenga Jumba la Sanaa (Theater Centre) ili vijana wa aina hii wawe na sehemu nzuri ya kuendesha shughuli zao?
(b) Kama Serikali inakubaliana na hoja hiyo, kituo hicho kitaanza kujengwa lini?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatambua mchango mkubwa wa wasanii mashuhuri wenye asili ya Mkoa wa Kigoma kama vile Diamond, Ali Kiba, Banana Zoro, Mrisho Mpoto japokuwa nimepata taarifa kwamba huyu Mrisho Mpoto origin yake ni Mkoa wa Ruvuma na wengine ambao wameiletea sifa na kuitambulisha nchi yetu katika fani ya muziki na sanaa.
Mheshimiwa Spika, katika Sera ya Utamaduni ya mwaka 1999, Sura ya 4, kipengele Na.4.1.9 inasema, Serikali itahakikisha kuwa panakuwa na jengo la kisasa la sanaa za maonesho katika ngazi ya Taifa. Aidha, wananchi watahamasishwa kuhakikisha kwamba wanatenga maeneo ya maonesho.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inaendelea kuhimiza Halmashauri na Manispaa zote nchini kutenga maeneo ya kujenga vivutio vya sanaa. Kuhusu Mkoa wa Kigoma, tunashauri Serikali ya Mkoa kwa kushirikisha Halmashauri zote za Mkoa huo ione umuhimu na namna bora ya kupanga na kutekeleza ujenzi wa Jumba la Sanaa. Aidha, tunatoa wito kwa Halmashauri zote nchini zione umuhimu wa kujenga majengo hayo.
(b) Mheshimiwa Spika, kazi ya kujenga miundombinu katika Halmashauri mbalimbali nchini ni jukumu la Halmashauri husika. Hivyo kila Halmashauri inashauriwa kutenga fedha katika bajeti zao kwa ajili ya Maendeleo ya Sanaa.
MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:-
Jimbo la Nyamagana ni jimbo pekee lililochangia mradi wa ujenzi wa nyasi bandia kupitia TFF shilingi 160,000,000.
Je, ni lini Serikali itawasisitiza TFF kuhakikisha kuwa uwanja huu unakamilika kwa wakati na kuendeleza malengo yaliyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Shing‟oma Mabula, Mbunge wa Nyamangana kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, uboreshaji wa uwanja wa Nyamagana wa kuweka nyasi bandia ulianza mwaka 2014 ukiwa na thamani ya dola za Kimarekani 737,886 sawa na shilingi za Kitanzania 1,193,161,662. Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Mpira wa Miguu (FIFA) lilitoa msaada kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) kiasi cha dola za Kimarekani 618,946 sawa na shilingi za Kitanzania 1,000,835,682 na Halmashauri ya Nyamangana ilichangia dola za Kimarekani 118,943 sawa na shilingi za Kitanzania 192,330,831.
Mheshimiwa Naibu Spika, nyasi hizo bandia zimegharimu tozo kiasi cha dola za Kimarekani 100,121.93, sawa na shilingi za Kitanzania 220,268,400 ikujumuisha import duty na VAT. TFF kama msimamizi wa mpira wa miguu kwa niaba ya Halmashauri ya Nyamangana na Serikali, wameshughulikia mchakato wa kutoa msamaha wa tozo hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nyasi bandi tayari zimewasili Dar es Salaam tangu tarehe 17 Aprili, 2016. Baadhi ya vifaa tayari vimeshafika katika Uwanja wa Nyamagana na mkandarasi amekwishaanza kazi ya ukarabati wa uwanja huo. TFF sasa wako katika mchakato wa kumalizia kusafirisha vifaa vilivyobaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ukweli kwamba ukarabati wa uwanja wa Nyamagana kuufanya uwe wa nyasi bandia unahitaji umakini mkubwa ili uwe mzuri, imara na wenye hadhi ya Kimataifa ni lazima mkandarasi ahakikishe kuwa ubora wa viwango vinazingatiwa. Kwa vile mpango wa ukarabati huo ulitakiwa ukamilike mwishoni mwa mwezi huu, natoa wito kwa mkadarasi huyo kuhakikisha kwamba ukarabati huo unakamilika haraka iwezekanavyo ili uweze kutumika.
MHE. COSTANTINE J. KANYASU aliuliza:-
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF) kupitia mtandao wa Twitter alitangaza kuzuia timu yoyote katika kundi „C‟ la Ligi Daraja la Kwanza kupanda daraja kabla ya mechi zao kukamilika na kabla ya vikao halali vya uchaguzi kufanyika:-
Je, Serikali haioni kwamba, maamuzi yalifanywa kinadharia na uonevu mkubwa kwa Timu ya Geita Gold Sport?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Costantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, maamuzi yaliyofanywa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF) dhidi ya Timu ya Geita Gold Sports ya kuishusha Daraja kutoka la Kwanza kwenda la Pili hayakuwa ya kinadharia au uonevu. Yalizingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo katika kushughulikia malalamiko yanayotokana na mwenendo wa mashindano husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa TFF baada ya kupata malalamiko kutoka timu za Kundi „C‟ kuhusu timu ya Geita Gold Sports kukiuka Kanuni za Mashindano ya Ligi Daraja la Kwanza kwa kujitangazia kuwa ni washindi katika kundi hilo hata kabla haijakamilisha kucheza mechi moja, iliielekeza Kamati ya Nidhamu kufanya uchunguzi wa suala hilo na kuchukua hatua stahiki. Kupitia vikao vya maamuzi vilivyokaa kujadili suala hilo ilionekana kuwa, timu ya Geita Gold Sports imekiuka Kanuni za Ligi na hivyo ilistahili kupewa adhabu ya kushushwa kutoka Daraja la Kwanza hadi la Pili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wa TFF anao utaratibu wa kuvitahadharisha vilabu vinavyoshiriki mashindano ya ligi katika ngazi mbalimbali kuzingatia sheria, kanuni na taratibu, ili kuepuka migogoro isiyokuwa ya lazima hivyo, taarifa aliyoitoa kupitia mtandao wa twitter ilikuwa ni sehemu ya tahadhari hiyo. Aidha, napenda kuchukua fursa hii kuvitaka Vyama vya Michezo, Mashirikisho, Vilabu na wadau kwa ujumla kuzingatia Katiba, Sheria, Kanuni na Taratibu zilizowekwa katika kuongoza na kusimamia utekelezaji wa mipango, maamuzi, chaguzi mbalimbali kwa maslahi ya vyombo hivyo na Taifa kwa ujumla.
MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Matumizi yasiyo sahihi ya lugha ya Kiswahili kwenye vyombo vya habari hayatoi fursa ya kukua kwa lugha yetu na badala yake yanachangia kurithisha lugha yetu kwa watoto kwa namna iliyo mbovu; mathalani, Mtangazaji wa runiga au redio anasema “hichi” badala ya “hiki” au nyimbo hii badala ya “wimbo huu” na kadhalika.
Je, Serikali ina mpango gani wa kimkakati wa kuvifanya vyombo vya habari kuwa mawakala wa kulinda usahihi wa lugha ya Kiswahili badala ya kuwa miongoni mwa wabomoaji wa lugha yetu?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea kusimamia na kuratibu matumizi ya Kiswahili fasaha kwa vyombo vya habari. Hivi sasa inaandaliwa Sera ya Lugha ambayo itabainisha majukumu ya vyombo vya habari katika matumizi na uendelezaji wa lugha ya Kiswahili. Aidha, kwa sasa hatua mbalimbali zinachukuliwa katika kuhakikisha kuwa vyombo vya habari vinakuwa mawakala wa kulinda lugha ya Kiswahili, ambapo Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) kwa kushirikiana na wadau wa Kiswahili limeendelea kuendesha semina, warsha, makongamano na kutoa elimu inayohusu matumizi fasaha ya Kiswahili kwa waandishi wa vyombo vya habari mbalimbali pamoja na kuandika makala na vijitabu maalum na kuvisambaza kwa wanahabari kuhusu matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa lugha ya Kiswahili ni utambulisho na utamaduni wa Taifa letu na vile vile ndiyo lugha ya Taifa, waandishi wa habari wanalo jukumu kubwa la kuhakikisha lugha hii inaendelezwa ipasavyo, ikiwa ni pamoja na kuzingatia matumizi sahihi.
Aidha, mifano iliyotolewa na Mheshimiwa Mbunge ya “wimbo huu” na “hiki” ni mada za nomino na sarufi ambazo hufundishwa katika somo la Kiswahili katika shule za msingi na upili. Hivyo, napenda kutoa wito kwa wanafunzi ambao miongoni mwao ni wanahabari watarajiwa kujifunza masomo yote kwa bidii ikiwa ni pamoja na Kiswahili.
Vilevile wamiliki wa vyombo vya habari wazingatie ufaulu wa somo la Kiswahili kama moja ya sifa kwa waombaji wa kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwashauri wanahabari kutumia zana kama vile kamusi na vitabu vya miongozo ya uandishi na kuhudhuria makongamano ya Kitaifa na ya Kimataifa ya lugha ya Kiswahili, kwa mfano, Chama cha Kiswahili Afrika Mashariki (CHAKAMA) na Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili Afrika Mashariki (CHAWAKAMA) ambayo hufanyika mwezi Septemba kila mwaka. Katika makongamano hayo, masuala ya kisarufi na ya kifasihi huwasilishwa na kujadiliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii itawasaidia kuongeza ujuzi na weledi wa lugha ya Kiswahili, kujua pia istilahi za kisayansi na kiteknolojia na hivyo kuandika na kutangaza kazi bora na zenye maudhui lengwa kwa jamii na kuepuka upotoshaji wa maneno ya Kiswahili usio wa lazima.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapunguzia wasanii gharama
za ukaguzi wa filamu ambapo kwa hivi sasa gharama hizo ni shilingi elfu moja
kwa dakika?
(b) Je, Bodi ya Filamu imejipanga kwa kiasi gani kuhakikisha huduma
zake zinatambulika nchi nzima tofauti na sasa ambapo ni wasanii wachache wa
filamu ndiyo wanafahamu wajibu na majukumu wa Bodi hiyo ambayo hata ofisi
zake hazijulikani ipasavyo sehemu zilipo Jijini Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi,
Mbunge wa Mafinga Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ada za uhakiki kwa nchi yetu zipo kwa
mujibu wa sheria na kanuni. Gharama hizi hulipwa kwa nakala mama tu (master)
baada ya hapo mtayarishaji huzalisha nakala kwa idadi anayohitaji. Nchi yetu
hutoza ada ambazo ni rafiki ukilinganisha na nchi nyingine. Kwa mfano, Nigeria
ambayo ni nchi iliyopiga hatua kubwa kwa upande wa filamu hutoza filamu
yenye urefu wa dakika 60 ambayo ni filamu ya lugha ya asili kwa naira 30,000
sawa na zaidi ya dola 150 ambayo ni sawa na Sh. 337,950 kwa viwango vya
ubadilishaji vya Sh. 2,253 kwa dola na Kenya ni sawa na Sh.190,000 za Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu hutoza filamu za Kitanzania zenye
urefu wa dakika 60 kwa Sh.60,000 sawa na Sh.1,000 kwa dakika. Gharama hizi ni
asilimia 18 ya zile za Nigeria na asilimia 32 ya zile za Kenya. Kwa maana hiyo, ni
wazi kwamba Tanzania hutoza ada ambayo ni nafuu na rafiki.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Bodi ya Filamu imeendelea kujitangaza
kwa wadau kupitia shughuli mbalimbali za Kitaifa na Kimataifa. Mfano kushiriki
katika Maonesho ya Sabasaba, Nanenane, Wiki ya Vijana na Kilele cha Mbio za
Mwenge wa Uhuru na Jumuiya ya Afrika Mashariki Utamaduni Festivals. Vilevile
Bodi inatumia vyombo mbalimbali vya habari ikiwemo TBC1, E-FM, Clouds Media,
Gazeti la Mtanzania na kadhalika. Pia Bodi imekuwa ikifanya warsha za
kuwajengea wadau weledi katika masuala ya filamu sehemu mbalimbali
ikiwemo mikoa na wilaya ambapo ni sehemu ya kujitangaza. Aidha, Bodi
inakamilisha tovuti yake ambayo itasaidia kujitangaza na itaendelea kutumia
vyombo vya habari, machapisho na warsha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Bodi za Mikoa na Wilaya ambazo
zinafanya majukumu ya Bodi katika ngazi za Mikoa na Wilaya. Wizara kwa kushirikiana na TAMISEMI itaendelea kuimarisha Bodi za Mikoa na Wilaya ili ziweze
kutoa huduma kwa wigo mpana zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ofisi za Bodi awali zilikuwa Barabara ya
Morogoro, Jengo la Textile ambapo hapakuwa rafiki kwa wadau. Mwaka 2012,
Wizara ilihamisha ofisi za Bodi kwenda Mtaa wa Samora, Jengo la Shirika la
Nyumba, Plot No. 2271/32 ambapo zipo Ofisi za Habari Maelezo mkabala na Tawi
la Benki ya NMB, ghorofa ya kwanza.
MHE. MAULID S. MTULIA Aliuliza:-
Taifa lina tatizo kubwa la ukosefu wa ajira rasmi kwa vijana. Vijana wa Jimbo la Kinondoni wameamua kujiajiri katika sanaa mbalimbali kama vile maigizo, maonesho ya mitindo na michezo mbalimbali:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea vijana hawa vifaa, mitaji na menejimenti ili kuongeza tija katika kazi zao;
(b) Je, Serikali imefikia wapi katika suala la hatimiliki ili Wasanii, Wanamichezo na Wanamitindo wetu waweze kupata haki zao.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA
MICHEZO Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maulid Said Mtulia, Mbunge wa Kinondoni, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, nianze wa kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote kwa kutambua mchango wa sanaa mbalimbali kama sehemu ya chanzo cha ajira kwa vijana wetu kama Mheshimiwa Maulid Said Mtulia, Mbunge ambaye amelionesha hilo katika Jimbo lake la Kinondoni. Wizara yangu kwa sasa iko katika mchakato wa kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Sanaa, ambapo dhima kubwa ya mfuko huo ni kusaidia kuinua kipato, kuongeza tija, kukuza uwezo na weledi kupitia utaratibu wa upatikanaji fedha utakaowekwa na hivyo kuwawezesha wasanii kuzalisha kazi bora za sanaa zenye kukidhi viwango vya masoko ya ndani na ya nje.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki ambacho Mfuko wa Maendeleo ya Sanaa unaandaliwa, Serikali inashauri Halmashauri zote ziwasaidie vijana wanaojishughulisha na sanaa kwa kuwapa mikopo yenye masharti na riba nafuu kwa ajili ya mitaji kutoka kwenye asilimia 10 ya mapato ya kila Halmashauri kwa kuwa sanaa pia ni sehemu ya ujasiriamali na ni chanzo kikubwa cha ajira kwa vijana wetu kwa sasa. Aidha, sekta binafsi, mashirika, Serikali za Mitaa na taasisi mbalimbali zinaombwa kushirikiana nasi katika kuinua, kukuza na kuboresha vipaji kwa wasanii ili
waweze kujikwamua kiuchumi.
(b) Kuhusu Hakimiliki, Wizara yangu kupitia Bodi ya Filamu, COSOTA na BASATA zimeendelea kuwaelimisha wasanii wa fani mbalimbali kuzisajili kazi zao ili ziweze kutambuliwa, kupata udhibiti na ulinzi kutokana na wizi wa kazi za sanaa. Aidha, Serikali imeendelea kushughulikia migogoro na biashara haramu ya kudurufu kazi za sanaa ili wasanii waweze kuongeza kipato chao.
Mheshimiwa Spika, haki na maslahi ya wasanii yanalindwa kwa Sheria Na. 7 ya mwaka 1999 ya Hakimiliki na Hakishiriki, Sheria Na. 4 ya Filamu na Michezo ya Kuigiza ya 1976 na Sheria Na. 23 ya Baraza la Sanaa la Taifa ya 1984. Serikali inaendelea na urasimishaji wa tasnia ya filamu na muziki ambapo kazi za wasanii hawa zinawekwa stempu za TRA ambazo huwezesha kubaini nakala halisi. Serikali na taasisi zake itaendeleza zoezi la urasimishaji kwa fani nyingine.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza:-
Uwanja wa mpira wa miguu Lindi ulijengwa tangu mwaka 1957 wakati wa ukoloni wa Gavana Sir Edward Twining na mpaka leo haujafanyiwa maboresho.
Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuukarabati na kuwa wa kisasa ukizingatiwa kwamba uwanja huo ulikuwa ukitumika kwa ajili ya michezo ya Afrika Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge Viti Maalum. kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uwanja wa mpira wa miguu wa Lindi (Ilula) ni mkongwe ulijengwa wakati wa ukoloni wa Mwingereza na unahitaji ukarabati ili kuufanya kuwa wa kisasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Maendeleo ya Michezo inahimiza kila taasisi yenye kiwanja au viwanja vya michezo kuvitunza viwanja hivyo ili viweze kudumu. Uwanja huu upo chini ya Halmashauri ya Lindi kama ilivyo kwa viwanja vingine vingi vilivyoko chini ya Halmashauri hapa nchini. Wizara yangu inashauri Halmashauri ya Lindi kuangalia uwezekano wa kuufanyia ukarabati uwanja huo kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali pamoja na wananchi wa Lindi wakiongozwa na Waheshimiwa Wabunge.
Aidha, Wizara yangu itakuwa tayari kutoa ushauri wa kitaalamu ili kusaidia kukarabati uwanja huo na kuufanya kuwa wa kisasa na kutumiwa na wanamichezo wengi zaidi wa Mkoa huo na Taifa kwa ujumla.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Haki ya kupata taarifa ni haki ya msingi kwa kila Mtanzania na vyombo vyetu vya habari havina wakalimani wa lugha ya alama kwa ajili ya kuwawezesha viziwi kupata habari kwa uelewa uliotimilifu kama raia wengine.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa vyombo vya habari hasa tv vinaajiri wakalimani hasa katika taarifa za habari ili waweze kufuatilia matukio yanayooneshwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Amina Saleh Mollel (Mbunge), kwa kuona umuhimu wa suala hili pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote hasa Mheshimiwa Stella Alex Ikupa (Mbunge) ambaye naye aliuliza swali hili tarehe 08/05/2017 katika mjadala wa bajeti ya Wizara yetu.
Napenda kulitaarifu Bunge lako kuwa baada ya swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa Mbunge, Wizara iliitisha kikao cha wadau mbalimbali wakiwepo Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, VETA, Chama cha Wakalimani wa Lugha za Alama (TASLI), TBC na wadau wengine ili kutafakari namna ya kutekeleza kwa haraka azma hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mengine, tulikubaliana kwamba VETA watoe mafunzo hayo kwa kushirikiana na CHAVITA na TASLI, kutokana na mtandao mkubwa ambao VETA wanao na VETA wamekubali. TASLI wamepewa kazi ya kuandaa kanzi data za wakalimani wa lugha ya alama kwa viziwi, na TCRA wanaandaa kalenda yaani road map ya utekelezaji wa matumizi ya huduma za wakalimani wa lugha ya alama katika vituo vya televisheni nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na hatua hizo TBC inaendelea na mawasiliano yake na Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Sebastian Kolowa - Taasisi ya Elimu ya Juu, inayofundisha wataalamu wa lugha ya alama kuona ni namna gani shirika linavyoweza kuwatumia wataalamu, wahitimu na wanafunzi wa chuo hicho kutoa kwa muda huduma ya lugha ya alama kupitia TBC.
Aidha, Serikali imeandaa kutekeleza suala hili kwa kuweka wakalimani wa lugha ya alama katika matukio ya Kitaifa kama maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano yaliyofanyika 26 Aprili, 2017. Vilevile TBC iko kwenye mchakato wa kuajiri wakalimani wachache kwa kuanzia wa lugha za alama kwa taarifa zake za habari na katika matangazo machache yanayorushwa na televisheni hiyo ya TBC.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa wito kwa wamiliki wa vyombo vya habari binafsi nchini nao kuanza mchakato wa kuwaajiri wakalimani wa lugha ya alama ili waweze kuwawezesha watu wa kundi hili kupata taarifa kupitia vyombo vyao habari.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB aliuliza:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mawasiliano ya TBC Radio kwenye maeneo ya Tarafa ya Amani Muheza ni hafifu.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mawasiliano ya redio na televisheni ya Kituo cha Taifa cha TBC?
(b) Je, ni lini Serikali itaboresha mawasiliano kwenye maeneo hayo ya milima ya Amani ya Vituo vya Taifa Redio na TBC ili wananchi waweze kunufaika na vipindi hivyo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajab, Mbunge wa Muheza, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kuwa mawasiliano ya Redio na Televisheni ya Taifa (TBC) yanaimarishwa na kuwafikia wananchi katika maeneo yote ya nchi. Katika kutekeleza dhamira hiyo, Serikali kila mwaka imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya kuimarisha miundombinu na usikivu wa redio na televisheni ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali ilitenga kiasi cha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuboresha usikivu wa redio za Shirika katika maeneo ya mipakani mwa nchi ambayo ni Kakonko, Tarime, Rombo, Longido na Nyasa, na utekelezaji wa mradi huo unaendelea. Aidha, katika hatua ya kuhakikisha changamoto ya usikivu wa redio za Shirika inapatiwa ufumbuzi kwa kiwango kikubwa, Serikali imeendelea kuimarisha bajeti ya upanuzi wa usikivu wa TBC, ambapo katika mwaka 2017/2018 shilingi bilioni tatu zimetengwa ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni mbili ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2016/2017, ambapo kiasi cha shilingi bilioni moja zilitengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uimarishaji wa usikivu wa Redio na Televisheni ya Taifa ni wa hatua kwa hatua, hivyo Serikali itaendelea kutekeleza azma hii katika maeneo ambayo kuna usikivu hafifu kwa kuendelea kutenga fedha kila mwaka.
MHE. ALLY SALEH ALLY aliuliza:-
Tanzania imesajili michezo kadhaa ambayo huingia kwenye medani ya Taifa kiushindani lakini kote huwa ni mashamba yanayozaa visingizio.
(a) Je, Serikali haioni haja sasa ya kujipinda katika michezo michache kiushindani Kimataifa?
(b) Je, kama kukiwa na uamuzi huo inaweza kuwa michezo ipi?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imesajili michezo mbalimbali kwa kuzingatia sera, sheria, kanuni na taratibu zilizopo. Aidha, ili timu au mchezaji aweze kushiriki katika mashindano ya kimataifa kama vile michezo ya Olympic na michezo mingine, lazima awe amefikia viwango vilivyowekwa na mashirikisho ya kimataifa. Serikali inatoa mwanya kuibua na kukuzwa kwa vipaji katika michezo mbalimbali bila upendeleo. Suala la kufanya vizuri katika mashindano linategemeana na viwango vya uelewa, mazoezi, mafunzo na uzoefu katika mchezo husika.
Aidha, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali inatoa msaada wa hali na mali kufanikisha timu ama mchezaji aliyefikia viwango kushiriki michezo ya Kimataifa ikiwa taarifa na taratibu zinazingatiwa tangu ngazi za awali. Kitendo cha kuchagua michezo kadhaa kinaweza kupelekea kupoteza vipaji ambavyo havijavumbuliwa na kukuzwa kufikia kushiriki mashindano kitaifa na kimataifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo Serikali itaendelea kuhamasisha michezo yote kupitia vyama vya michezo kwa sababu kila mchezo unaweza kushiriki kiushindani. Hii inasaidia kutoa fursa kwa wanamichezo wenye vipaji tofauti kuweza kushiriki katika michezo ya kimataifa.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, maoni ya Mheshimiwa Mbunge ni mazuri kwa maana ya kujikita katika michezo ile ambayo tunadhani itaweza kusaidia Taifa kufanya vizuri katika ushindani kimataifa, hili litawezekana kwa kusaidia timu ama mchezaji aliyefuzu, kwani katika hali halisi huwezi kuamua kuwa huu ndio mchezo unaoweza kufanya vizuri bila kupata viwango.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, niseme kuwa kwa sasa bado utaratibu huu hatujaanza kuutumia na kwa hiyo sio rahisi kujua ni michezo gani kwani kila mchezo unaandaliwa kwa kufuata taratibu na viwango husika na matokeo mazuri yanapatikana kwa kuibua na kukuza vipaji. Kwa kuchagua michezo kadhaa tutakatisha tamaa ukuaji wa vipaji katika michezo mingine. Lakini bado iko fursa kama wadau kufanya upembuzi wa kina na kuja na maoni juu ya michezo gani tuipatie kipaumbele kwa manufaa ya Taifa.(Makofi)
MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:-
Waandishi wa Habari wanafanya kazi nzuri katika kuelimisha jamii.
Je, ni lini Serikali itaanzisha mfumo utakaotambua kazi zinazofanywa na tasnia ya habari?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kujibu swali hili, naomba uniruhusu nianze kwa kuipongeza timu yetu ya vijana ya Serengeti kwa ushindi wa mabao mbili kwa moja dhidi ya Angola jana nchini Gabon. (Makofi)
Vilevile nichukue nafasi hii kuwapongeza Watanzania wote kwa kushikamana na kushirikiana pamoja kuichangia na kuishangilia pamoja na kuitakia kheri timu yetu hii ya vijana ya Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huu mfupi, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Minja, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua na kuthamini kazi zinazofanywa na vyombo vya habari nchini. Mchango wa tasnia ya habari ni mkubwa katika kuhabarisha, kuelimisha na kuburudisha jamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua mchango huo, Serikali imeruhusu uwepo wa vyombo vya habari vya umma na sekta binafsi, yakiwemo makampuni binafsi, mashirika ya kidini na kijamii. Aidha, mchango wa vyombo vya habari unatokana na sera, sheria, mipango na taratibu zilizowekwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo unaotambua kazi za tasnia ya habari nchini upo tayari. Katika kudhihirisha hilo, Serikali ilitunga Sera ya Habari na Utangazaji ya mwaka 2003, Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 na sasa ina Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016 na Kanuni zake za mwaka 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri ya kuwezesha wanahabari kufanya kazi zao kwa weledi na kwa kuzingatia kanuni, sheria na taratibu ili kulinda amani na utulivu katika nchi yetu. Wizara yangu kwa sasa inaainisha mahitaji ya wataalamu katika tasnia ya habari ili kushirikiana na wadau wa ndani na nje tuweze kuwapatia mafunzo kwa lengo la kuboresha kazi zao.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
(a) Je, kuna vituo vingapi vinavyorusha matangazo kwa njia ya televisheni nchini na vinamilikiwa na Kampuni zipi?
(b) Je, ni vituo vingapi vinarusha matangazo ya televisheni bure kwa wananchi kupitia ving’amuzi?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO, alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya mawasiliano Tanzania imetoa leseni kwa vituo 32 vya Television hapa nchini. Orodha ya vituo hivyo na wamiliki wa vituo hivyo ni ndefu naomba nisiisome hapa ila nimekwishamkabidhi Mheshimiwa Mbunge na ninaomba iingie kwenye Hansard.
(b)Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania hutoa leseni ya maudhui ya utangazaji wa televisheni za aina mbili. Leseni za maudhui yanayotazamwa bila kulipia (free to air) na maudhui ya kulipia (pay tv). Aidha, leseni hizi zimegawanywa kimasoko. Kuna leseni za kitaifa ambazo hupaswa kuonekana nchi nzima na kuna leseni za kimkoa ambazo huruhusiwa kutangaza mikoa kumi ya Tanzania Bara na leseni za kiwilaya ambazo huonekana mkoa mmoja.
Mgawanyo huu wa kimasoko unatoa fursa kwa waombaji kutangaza maeneo wanayochangua kutokana na uwezo wao wa kifedha na na kiuendeshaji. Maudhui haya ya bila kulipia huonekana kupitia ving’amuzi vya Mkampuni ya Agape Associates Limited, Basic Transmission Limited na Star Media Tanzania Limited. Visimbuzi hivi ni TING, Startimes, DIGITEC na CONTINENTAL Vituo vyenye leseni ya soko la kitaifa ni TBC1, Channel 10, East Africa Televison, Independent Television, Star Television, Clouds TV na Bunge TV. Vituo vyenye soko la kimkoa ni TV Imaan, Agape TV (ATV) na TV1 zilizobaki zina soko la kiwilaya.
Aidha, Kituo cha TBC1 ambacho ni kituo cha umma (public broadcaster) kinapatikana bila malipo ya mwezi kwenye ving’amuzi vyote vya miundombinu isiyosimikwa ardhini yaani Digital Terrestrial Television na vile vinavyotumia mitambo ya satelite yaani direct to home kama vile Azam TV, DSTV na Zuku. Kituo cha TBC1 kinalazimika kuonekana bila malipo kwa mujibu wa masharti ya leseni za makampuni ya miundombinu ya utangazaji wa ardhini yaani DTT na Satelite (DTH).

ORODHA YA VITUO VYA TELEVISHENI NA WAMILIKI WAKE

1. Independent Television (ITV) - Reginald Mengi & Family Trust 99% & Reginald Abraham Mengi 1%
2. Star Television - Diallo Investment Co. Limited 50% & Nyalla Investment Co. Limited 50%
3. Channel Ten Television - Africa Media Group Limited 100%
4. TBC 1 - Tanzania Broadcasting Corporation 100%
5. TBC 2 - Tanzania Broadcasting Corporation 100%
6. East Africa Television (EATV) - Reginald Mengi & Family Trust 99% & Reginald Abraham Mengi 1%
7. Agape Television (ATV) - World Agape Ministries 100%
8. C2C Television - Africa Media Group Limited 100%
9. Dar es Salaam Television (DTV) - Africa Media Group Limited 100%
10. Abood Television - Aziz Mohammed Abood 50% & Fauzi Mohammed Abood 50%
11. CTN Television - Africa Media Group Limited 100%
12. Capital Television - Reginald Mengi & Family Trust 99% & Reginald Abraham Mengi 1%
13. Clouds TV - Joseph Mlebya Kusaga 50%, Andrew Dogan Kusaga 20% & Alex Kusaga Mkama 30%
14. VIASAT 1 Television - Dr. Gideon H. Kaunda 7.5%, Ambassador Paul Milyango Rupia 7.5% & Dr. Wilbert Basilius Kapinga 36%
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Timu yetu ya Taifa imeendelea kufanya vibaya katika michezo ya kimataifa. Je, Serikali imeliona hilo na imechukua hatua gani?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Methusalah Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikifanya juhudi katika kuendeleza michezo ili kuwa na timu bora za michezo katika ngazi mbalimbali hasa ngazo za timu za Taifa na baadhi ya juhudi hizo ni pamoja na:-
(i) Kuboresha mazingira ili wadau wa michezo wawekeze kisayansi katika michezo kuanzia umri mdogo kwa lengo la kugundua na kukuza vipaji na hatimaye kupata wachezaji mahiri wa timu za Taifa.
(ii) Kuendesha mafunzo mbalimbali ya michezo kwa wataalam wa michezo nchini katika Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya.
(iii) Kutoa mafunzo ya michezo mbalimbali ya muda mfupi kwa Wilaya na Mikoa kupitia Baraza la Michezo la Taifa.
(iv) Kutoa ushauri elekezi kwa vyama vya michezo wakati wa maandalizi ya timu za Taifa zinazoshiriki kwenye michezo ya Kimataifa mfano Olympiki, Michezo ya Afrika (All African Games) na michezo ya Jumuiya ya Madola.
(v) Serikali imetenga shule mbili kila Mkoa kama shule maalum za michezo na pia inaendelea kuhamasisha wadau kuanzisha shue za aina hiyo (sports academy).
(vi) Kuelekeza vilabu na vyama vya michezo kuwa na timu za umri wa chini na kuanzisha ligi zao kwa michezo hiyo.
(vii) Kushirikiana na Wizara nyingine kuendesha na kuratibu mashindano ya michezo kwa ajili ya wanafunzi wa shule za msingi (UMITASHUMTA) na ile ya shule za sekondari (UMISETA).
Mheshimiwa Spika, ili tufanikiwe katika hilo, Wizara inatoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya michezo katika maeneo yao ikiwa ni pamoja na zile za uibuaji wa vipaji na ujenzi wa miundombinu kwa kuhamasisha wadau mbalimbali. Aidha, Wizara inatoa wito kwa Halmashauri zote nchini kuendelea kuyalinda maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli za michezo na burudani pamoja na kuhakikisha mipango ya matumizi ya ardhi katika maeneo yao inazingatia utengwaji wa maeneo ya michezo na burudani.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itawapatia wananchi wa Kyerwa haki yao ya kusikiliza Redio ya Taifa (TBC Taifa) ili kujua yanayoendelea katika nchi yao kama ilivyokuwa hapo awali kabla ya kubadilisha teknolojia ya habari, badala yake sasa wanasikiliza redio za Rwanda na Uganda.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kyerwa iko katika Mkoa wa Kagera ambapo matangazo ya redio yanapatikana kupitia mtambo wa TBC ulioko katika Manispaa ya Bukoba. Mtambo huu unasafirisha mawimbi ya redio katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huu wa Kagera ikiwemo wananchi wa Jimbo la Kyerwa. Usikivu wa TBC katika eneo hili umeshuka na kusababisha baadhi ya maeneo kukosa matangazo ya redio ikiwemo Jimbo la Kyerwa. Ili kuimarisha usikivu katika maeneo ya mipakani ikiwemo Wilaya ya Kyerwa, mpango wa TBC ni kujenga mitambo ya FM katika maeneo haya ili wananchi wake waweze kupata matangazo kutoka redio yao ya Taifa TBC.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa na kama ilivyobainishwa katika hotuba ya Bajeti ya Wizara ya mwaka 2017/2018 TBC imeanza kutekeleza mpango huu katika Wilaya na maeneo ya Kibondo, Nyasa, Longido, Tarime na Rombo na itaendelea katika wilaya nyingine ikiwemo Wilaya ya Kyerwa kadri bajeti inavyoendelea kuimarika.
MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:-
Mchango wa kazi za wasanii umeonekana katika kutoa ajira lakini bado wasanii wanakabiliwa na changamoto mbalimbali za kuhujumiwa kazi zao ambapo Mheshimiwa Rais ametoa maagizo mbalimbali ya kushughulikia watu wanaohujumu kazi za wasanii.
Je, mpaka sasa ni hatua gani zimechukuliwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijajibu swali la Mheshimiwa Devotha naomba kwa ruhusa yako nichukue nafasi hii kutoa taarifa fupi ya mafanikio ya mrembo Aisha Mabula ambaye tulimuona hapa hivi karibuni Bungeni, aliewezeshwa na Waheshimiwa Wabunge kushiriki mashindano ya ulimbwende ya Miss World Super Model nchini China.
Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya washiriki walikuwa 52 kutoka nchi mbalimbali duniani lakini kutoka Afrika ni wawili ambapo mmoja wao ni huyo Bi. Aisha Mabula na Aisha Mabula alifanikiwa kuingia 14 bora kama fainali na katika fainali hiyo alishika nafasi ya tisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza Bi. Aisha kwa kuiwakilisha vizuri nchi yetu ya Tanzania pamoja na Bara la Afrika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee kabisa niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa moyo wenu wa ukarimu ambapo mlimchangia na kumuwezesha kushiriki katika mashindano hayo ya kidunia ambayo naamini kabisa mafanikio haya yatamuwezesha kupata ajira na kuendelea kuitangaza nchi yetu Kimataifa na hasa katika sekta ya utalii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huu mfupi naomba sasa kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia Kamati ya Urasimishaji wa Kazi za Filamu na Muziki nchini inayojumuisha Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Bodi ya Filamu Tanzania (TFB) na Chama cha Hakimiliki Tanzania (COSOTA) hutoa miongozo mbalimbali kuhusiana na masuala ya ulinzi na kazi za sanaa.
Aidha, kwa kushirikiana na COSOTA Wizara kupitia BASATA na Bodi ya Filamu Tanzania (TFB) hutoa copyright clearance certificate kwa mmiliki wa kazi yoyote ya sanaa kabla ya kupewa stempu ya kodi ya TRA. Lengo la stempu hizo ni kurasimisha sekta ya filamu na muziki katika uuzaji wa CD, DVD, kanda na kadhalika na hivyo kukabiliana na hujuma katika kazi za wasanii.
Mheshimiwa Naibu Spika, pale ambapo sheria na taratibu za forodha na za kulinda hakimiliki zinakiukwa na hivyo kuathiri maslahi ya wasanii, Serikali huendesha operesheni za kukamata kazi hizo za sanaa zenye utata. Hadi kufikia Machi 2017, Wizara ilifanya operesheni kubwa mbili na za kawaida sita dhidi ya filamu zinazoingia sokoni bila kufuata utaratibu ambapo jumla ya kazi 2,394,059 zilikamatwa zikiwemo kazi za nje ya nchi 2,393,529 zenye thamani ya zaidi ya shilingi 3,590,293,500 na za ndani 530 zenye thamani ya shilingi 1,590,000.
Aidha, mitambo ya kufyatua kazi za filamu (duplicators) 19, printers za CD/DVD nane, DVD writers 31, kompyuta tatu na UPS saba zilikamatwa katika operesheni hizo.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Haki ya kupata taarifa ni haki ya msingi kwa kila Mtanzania na vyombo vyetu vya habari havina wakalimani wa lugha ya alama kwa ajili ya kuwawezesha viziwi kupata habari kwa uelewa uliotimilifu kama raia wengine.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa vyombo vya habari hasa tv vinaajiri wakalimani hasa katika taarifa za habari ili waweze kufuatilia matukio yanayooneshwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Amina Saleh Mollel (Mbunge), kwa kuona umuhimu wa suala hili pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote hasa Mheshimiwa Stella Alex Ikupa (Mbunge) ambaye naye aliuliza swali hili tarehe 08/05/2017 katika mjadala wa bajeti ya Wizara yetu.
Napenda kulitaarifu Bunge lako kuwa baada ya swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa Mbunge, Wizara iliitisha kikao cha wadau mbalimbali wakiwepo Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, VETA, Chama cha Wakalimani wa Lugha za Alama (TASLI), TBC na wadau wengine ili kutafakari namna ya kutekeleza kwa haraka azma hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mengine, tulikubaliana kwamba VETA watoe mafunzo hayo kwa kushirikiana na CHAVITA na TASLI, kutokana na mtandao mkubwa ambao VETA wanao na VETA wamekubali. TASLI wamepewa kazi ya kuandaa kanzi data za wakalimani wa lugha ya alama kwa viziwi, na TCRA wanaandaa kalenda yaani road map ya utekelezaji wa matumizi ya huduma za wakalimani wa lugha ya alama katika vituo vya televisheni nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na hatua hizo TBC inaendelea na mawasiliano yake na Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Sebastian Kolowa - Taasisi ya Elimu ya Juu, inayofundisha wataalamu wa lugha ya alama kuona ni namna gani shirika linavyoweza kuwatumia wataalamu, wahitimu na wanafunzi wa chuo hicho kutoa kwa muda huduma ya lugha ya alama kupitia TBC.
Aidha, Serikali imeandaa kutekeleza suala hili kwa kuweka wakalimani wa lugha ya alama katika matukio ya Kitaifa kama maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano yaliyofanyika 26 Aprili, 2017. Vilevile TBC iko kwenye mchakato wa kuajiri wakalimani wachache kwa kuanzia wa lugha za alama kwa taarifa zake za habari na katika matangazo machache yanayorushwa na televisheni hiyo ya TBC.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa wito kwa wamiliki wa vyombo vya habari binafsi nchini nao kuanza mchakato wa kuwaajiri wakalimani wa lugha ya alama ili waweze kuwawezesha watu wa kundi hili kupata taarifa kupitia vyombo vyao habari.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB aliuliza:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mawasiliano ya TBC Radio
kwenye maeneo ya Tarafa ya Amani Muheza ni hafifu.
• Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mawasiliano ya redio na televisheni ya Kituo cha Taifa cha TBC?
• Je, ni lini Serikali itaboresha mawasiliano kwenye maeneo hayo ya milima ya Amani ya Vituo vya Taifa Redio na TBC ili wananchi waweze kunufaika na vipindi hivyo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajab, Mbunge wa Muheza, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kuwa mawasiliano ya Redio na Televisheni ya Taifa (TBC) yanaimarishwa na kuwafikia wananchi katika mmaeneo yote ya nchi. Katika kutekeleza dhamira hiyo, Serikali kila mwaka imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya kuimarisha miundombinu na usikivu wa redio na televisheni ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali ilitenga kiasi cha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuboresha usikivu wa redio za Shirika katika maeneo ya mipakani mwa nchi ambayo ni Kakonko, Tarime, Rombo, Longido na Nyasa, na utekelezaji wa mradi huo unaendelea. Aidha, katika hatua ya kuhakikisha changamoto ya usikivu wa redio za Shirika inapatiwa ufumbuzi kwa kiwango kikubwa, Serikali imeendelea kuimarisha bajeti ya upanuzi wa usikivu wa TBC, ambapo katika mwaka 2017/2018 shilingi bilioni tatu zimetengwa ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni mbili ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2016/2017, ambapo kiasi cha shilingi bilioni moja zilitengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uimarishaji wa usikivu wa Redio na Televisheni ya Taifa ni wa hatua kwa hatua, hivyo Serikali itaendelea kutekeleza azma hii katika maeneo ambayo kuna usikivu hafifu kwa kuendelea kutenga fedha kila mwaka.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-
Wanariadha wa baadhi ya nchi ambazo kijiografia mazingira yao yanafanana na baadhi ya maeneo katika nchi yetu wamekuwa wakishiriki katika mashindano ya riadha ya majiji makubwa duniani kama vile New York Marathon, Tokyo Marathon na kadhalika na hivyo kuzitangaza nchi zao ipasavyo.
Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kuwa inafufua mchezo wa riadha ili kutumia kutangaza utalii wa nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuwa baadhi ya nchi zimekuwa zikifanya vizuri katika mashindano makubwa duniani na hivyo kuzitangaza nchi zao ipasavyo. Hata hivyo, nchi yetu imeanza kufanya vizuri katika mashindano ya riadha kama ilivyokuwa katika miaka ya nyuma kupitia kwa wanariadha wake kama vile Francis Naal, Samson Ramadhani, Gidamis Shahanga, Juma Ikangaa, Suleiman Nyambui na Filbert Bayi. Mathalani, nchi yetu imeweza kupata mafanikio katika riadha hivi karibuni kupitia wanariadha wake kama ifuatavyo:-
(a) Alphonce Simbu aliyekuwa mshindi wa kwanza na kupata medali ya dhahabu kwenye mashindano ya Standard Chartered Mumbai Marathon, India tarehe 15 Januari, 2017;
(b) Cecilia Ginoka Panga aliyeshinda Beijing International Half Marathon yaliyofanyika tarehe 16 Aprili, 2017; na
(c) Emmanuel Giniki Gisamoda aliyeshinda Shanghai International Half Marathon yaliyofanyika tarehe 23 Aprili, 2017.
Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kuleta maendeleo endelevu ya mchezo wa riadha na michezo yote kwa ujumla, pamoja na mambo mengine, Wizara inakamilisha mapitio ya Sera ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995 ili kuhakikisha inaendana na mahitaji ya sasa katika maendeleo ya michezo ikiwemo kuimarisha uendeshaji na usimamizi katika ngazi zote, ugharamiaji pamoja na uibuaji na uendelezaji wa vipaji katika ngazi mbalimbali.
Aidha, Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeendesha mashindano ya UMISETA na UMITASHUMTA ambayo pamoja na mambo mengine, yanalenga kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana wetu katika mchezo wa riadha. Aidha, hivi sasa Wizara yangu inakamilisha taratibu za kuandaa miongozo ya Kiserikali ili kuwezesha wadau wote kuendesha kuendesha shughuli zao katika mazingira ya weledi na stadi bora za michezo.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia kwa kushirikiana na wadau inatekeleza programu mbalimbali za kuendeleza mchezo wa riadha nchini ikiwemo Kilimanjaro Marathon, Bagamoyo Marathon, Tulia Marathon, Heart Marathon na kadhalika ambayo hushirikisha wanarisha kutoka ndani na nje ya nchi. (Makofi)