Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Amina Saleh Athuman Mollel (2 total)

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali kwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, baadhi ya walimu wenye ulemavu kutegemeana na ulemavu walionao wanahitaji vifaa maalum vya kujifunzia na kufundishia katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Vifaa hivyo ni pamoja na mashine za maandishi ya nukta nundu, shime sekio pamoja na vifaa vingine. Natambua kazi nzuri iliyofanywa ofisi yako pia Wizara ya Elimu kwa kutoa vifaa kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum. Bado tatizo lipo kwa walimu hasa kwa kuzingatia kwamba sio walimu wote wenye ulemavu wanaopangiwa kwenye shule zenye mahitaji maalum ambazo shule hizo zina vifaa hivi.

Je, wewe kama Baba na hasa kwa kuzingatia masuala haya ya watu wenye ulemavu yako chini ya ofisi yako, nini kauli yako ili kuhakikisha kwamba walimu hawa wanatekelezewa mahitaji yao na kutimiza majukumu yao pasipo matatizo yoyote?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina uratibu mzuri sana wa kuhahakisha kwamba Watanzania wenzetu wenye mahitaji maalum wanapata huduma stahiki ili waweze kukamilisha shughuli zao za siku katika nyanja mbalimbali. Moja kati ya ushahidi kwamba jambo hili limeratibiwa vizuri Serikali zote zilizopita pamoja na hii ya Awamu ya Tano tumeweza kutenga Wizara inayoshughulikia Watanzania wenzetu ambao wana mahitaji maalum. Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo mimi mwenyewe nipo, ndio hasa Wizara ambayo inashughulikia kwa ujumla wake, lakini tuna Wizara ya Elimu na Ofisi ya Rais (TAMISEMI) zote hizi zinaratibu kwa namna ambavyo tumepanga utaratibu wa kufikisha huduma hii mahali hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hawa wote ambao wana mahitaji maalum, tunatambua kwamba wakati wote wanahitaji kujielimisha, kupitia taasisi na shule mbalimbali na kule wako waelimishaji ambao wanafanya kazi hiyo kila siku. Sisi tuna utaratibu kwenye maeneo haya ya vyuo, taasisi na shule mpango wa kwanza tumepeleka fedha za kuwahudumia pale ambapo wanahitaji huduma kulingana na mahitaji yake. Wako wale ambao hawana usikivu mzuri, uono hafifu, ulemavu wa viungo, wote hawa tumewaandalia utaratibu kwa kupeleka fedha kwenye Halmashauri ili waweze kuhudumiwa. Pia walimu ambao wanatoa elimu hii nao pia tumeweza kuwawezesha kwa kuwapa vifaa vya kufundishia na kujifunzia kulingana na aina ya mahitaji ambayo tunayo.

Pia walimu hawa tunawapeleka semina mara nyingi kuhakikisha kwamba na wao pia wanapata elimu ya kisasa zaidi ili kuweza kuwahudumia vizuri hawa wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lini Serikali itajiimarisha katika kutoa huduma hii ni kwamba Serikali imeandaa kituo cha Msimbazi Center kuwa ni eneo la kukusanyia vifaa ambavyo tunavisambaza kwenye shule na taasisi zote ili viweze kutumika katika kufundishia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie pia Jumanne wiki ijayo napokea vifaa vingi sana vya elimu kule Dar es Salaam ambavyo vimeletwa kwa ajili ya kupeleka kwenye shule zetu za msingi. Miongoni mwa vifaa ambavyo pia tutakabidhiwa siku ya Jumanne ni pamoja na vifaa vya Watanzania wenzetu walioko vyuoni, kwenye shule ambao wana mahitaji maalum.

Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Amina Mollel na tunajua jitihada zako za kusemea sana eneo hili kwamba Serikali iko pamoja, Serikali inaendelea kuratibu vizuri na niendelee kukuhakikishia kwamba Serikali itaendelea kuratibu na kuhakikisha kwamba vifaa vya kujifunzia na kufundishia vitapatikana na hawa waelimishaji wanapata elimu ya mara kwa mara ili waweze kuwasaidia hawa wenzetu ambao wana mahitaji maalum. Ahsante sana.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Swali langu ninapenda kufahamu, kwa kuwa takwimu za Taifa kwa sasa zinaonyesha kuwa kila mwaka watu 82,000 wanaambukizwa virusi vya UKIMWI hapa nchini na ni-declare interest kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati ya UKIMWI na Dawa za Kulevya.

Mheshimiwa Spika, kati ya hao wanaoambukizwa ni kuanzia miaka 15 mpaka 64 na asilimia kubwa inaonyesha kwamba vijana ndiyo wanaoongoza hivi sasa kwa asilimia 40 na kati ya hao vijana, watoto wa kike ndiyo ambao wanaoongoza kwa asilimia kubwa.

Mheshimiwa Spika, watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI kwa sasa, takwimu za Taifa…

SPIKA: Sasa swali Mheshimiwa Mollel.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, swali langu; nilipenda kufahamu mkakati wa Serikali, tamko la Serikali juu ya hali hii kwa sababu hali ni mbaya. Nini tamko la Serikali katika kusaidia Taifa na hasa vijana ambao ndiyo tunawategemea katika nguvu kazi ya Taifa?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Mollel, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tatizo la UKIMWI nchini limekuwa likiratibiwa vizuri sana na Serikali toka tulipoanza kampeni ya kupambana na maambukizi ya UKIMWI kwa kushirikisha Wizara zote ambazo zinahusika katika kulinda afya ya Mtanzania. Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo hasa inasimamia suala la mapambano dhidi ya UKIMWI kwa kuwa tumeshaunda Taasisi inayoitwa TACAIDS. Tunafanya kazi kwa pamoja na Wizara ya Afya ambayo ndiyo ina wajibu wa kusimamia afya ya Mtanzania.

Mheshimiwa Spika, pia Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Kamati ya Kudumu ya Bunge ambayo inashughulikia masuala ya UKIMWI nayo pia imekua ikishiriki kikamilifu. Kwa hiyo, mkakati huu wa pamoja ndiyo unaowezesha sasa kupambana na maambukizi ya UKIMWI ambayo sehemu kubwa yanaathiri sana maisha ya vijana kama ambavyo umeeleza na takwimu ambazo unazo mezani kwako.

Mheshimiwa Spika, muhimu zaidi ni kwamba mkakati wetu sasa ambao tunao ni kuhakikisha kwamba wale Watanzania wote kwanza tunatakiwa kupima ili kujitambua afya yetu na malengo yetu kufikia mwaka 2020 kila Mtanzania awe ameshapima. Ndiyo maana tumeweka kampeni ya upimaji karibu maeneo yote na kila mahali wanapokutana, wananchi zaidi ya 100 lazima pawe na eneo la kupimia ili kutoa fursa kwa Watanzania kwenda kupima. Kwa hili pia tuna kampeni kubwa, tumegundua wanaopima sana ni akina mama kuliko wanaume, nami ni Balozi wa wanaume wa upimaji. Kwa hiyo, tunahamasisha kwa ujumla wake watu wapime.

Mheshimiwa Spika, pili, wale wote waliopima na wamegundulika kuwa na maambukizi, kufikia mwaka 2020 tunataka wote wawe wameshaanza kutumia dawa za kufubaza hivyo virusi vya UKIMWI. Tunataka kufikia mwaka huo kila ambaye amepima, akishajitambua aanze kutumia dawa. Malengo yetu ni wale wote ambao wamepima na kukutwa na virusi wawe wameanza kutumia dawa, ifikapo mwaka 2020 tupate idadi kubwa ya watu ambao tayari wamefubaza virusi vya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, nini ujumbe hapa? Ujumbe ni kwamba Serikali inaendelea na mkakati wa kuhakikisha kwamba tunapunguza kwa kiasi kikubwa maambuki ya UKIMWI nchini kupitia Kampeni, Kupitia Programu zetu ambazo tunazo, pia tunaendelea kuwaelimisha Watanzania kuendelea kutambua afya zao pale ambako wanajikuta wana maambukizi waende wakapime moja kwa moja na hasa vijana ambao umewalenga wa kati ya miaka 18 mpaka 25 ambayo sehemu kubwa ndio waathirika wakubwa hao ndio tunafanya kampeni.

Mheshimiwa Spika, hiyo kama haitoshi, tumeendelea kutoa elimu hii kwenye shule za msingi na sekondari ya maambukizi ya UKIMWI na kuwataka watoto sasa, vijana wetu kwenye shule za msingi na sekondari wawe na tahadhari ya maambukizi, waaache kujiingiza katika maeneo ambayo yana maambukizi ili waendelee kuwa salama na wao ndio wawe Walimu wa Watanzania wengine katika kujikinga na maambuki ya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo programu za kujikinga na UKIMWI zinaendelea na Serikali inaendelea na mpango wa kuwahamasisha Watanzania na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kupitia Kamati kazi nzuri wanayoifanya kuisaidia Serikali ya kuhakikisha kwamba Watanzania wanatambua umuhimu wa kupima, kupata madawa na umuhimu wa kujilinda wakati wote hapa tunapoendelea na shughuli zetu. Ahsante sana.