Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Amina Nassoro Makilagi (35 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu jioni ya leo. Vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu, muweza wa yote aliyeniwezesha kusimama kuweza kuzungumza jioni ya leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru sana sana wananchi wa Tanzania kwa kujua mchele ni upi na pumba ni zipi na kuchagua Chama cha Mapinduzi kwa ushindi wa kishindo kwa nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa upande wa Wabunge 73% na kwa upande wa Madiwani 74% na kwa upande wa Viti Maalum 80%, kwa kweli wananchi Mwenyezi Mungu awajalie sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoweza kusema hapa, tunawaahidi kwamba imani huzaa imani, tutaendelea kuwatumikia kwa moyo wetu wote na hata pale ambako Chama cha Mapinduzi hakikupata kura tutawahudumia bila ubaguzi likiwemo Jimbo la Arusha na Majimbo mengine ambako CCM haikushinda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nichukue nafasi hii kumpongeza sana, mpendwa wetu Rais wetu wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa jinsi alivyoanza kutekeleza kazi. Ameanza vizuri, anafanya kazi nzuri na kama kura zingepigwa leo ushindi wa CCM ungekuwa ni 69.999%. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya utangulizi huo, napenda sasa kujielekeza kwa mambo machache ambayo nimeyapanga kuyatilia mkazo katika hoja iliyo mbele yetu. Kwanza kabisa, naomba kuunga mkono hoja iliyo mbele yetu kwa sababu zifuatazo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu yangu ya kwanza ni kwamba, Waziri wa Fedha na timu yake yote wameandaa vizuri Mwelekeo wa Mpango wa mwaka 2016/2017. Ni Mpango unaoeleweka, wenye matumaini na ambao umelenga kuwakomboa Watanzania katika suala zima la kuwakomboa kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa sababu endapo Mpango huu utapangwa na ukatekelezwa, nina imani yale ambayo tumeyaandika kwenye Ilani ya CCM yataweza kufikiwa. Naomba sasa nitoe ushauri kwa mambo machache yafuatayo na nitaanza suala zima la ukusanyaji wa kodi. Ili mpango utakaotengenezwa usiendelee kubaki kwenye makaratasi, nilikuwa naishauri Serikali yetu hii ya CCM ijielekeze katika kuhakikisha inakusanya mapato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupongeza kazi nzuri ambayo imeanza kufanywa ya kukusanya mapato, lakini bado kuna baadhi ya mapato yanaishia mifukoni mwa watu, pia bado kuna mashine za kukusanyia mapato ni feki na bado kuna taasisi ambazo zinatumia vitabu ambavyo havieleweki katika mfumo wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba niishauri Serikali ili Mpango wa Maendeleo uweze kutekelezwa katika mwaka 2016/2017, lazima pia tuweke mkakati namna ambavyo Serikali itakusanya mapato. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nishauri Serikali yetu na Mawaziri wetu kwamba, katika kutekeleza Mpango huu, hauwezi kutekelezeka kama hawajadhibiti upotevu wa mapato na matumizi yasiyokuwa ya lazima. Naiomba sana Serikali yetu, ijielekeze katika kuhakikisha Mpango unaokuja 2016/2017 unalenga kwenda kuwakomboa Watanzania na hasa wanawake. Naomba Mpango unaokuja 2016, tujielekeze katika kuhakikisha suala zima la maji na hasa vijijini linapatiwa ufumbuzi ili wanawake wetu wanaotembea umbali mrefu waweze kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu, mwaka jana tulipanga mpango mzuri, lakini kwa bahati mbaya sana, hivi ninavyozungumza, sekta ya maji imepata asilimia nane tu ya bajeti. Sasa kama tutatengeneza mpango mzuri kama utakavyokuja na kama fedha hazikutafutwa na zikatengwa, Mpango wetu utabaki kwenye makaratasi na matokeo yake lengo ambalo limekusudiwa halitafikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba katika kuhakikisha Mpango unatekelezwa ni lazima tujielekeze sasa kuweka vipaumbele katika sekta ambazo zitaongeza mapato na napongeza mpango wa Serikali wa kuhakikisha tunafufua viwanda, tunaanzisha viwanda vipya na kukaribisha wawekezaji waje kuwekeza, lakini hapa naomba nitoe ushauri.
Naomba niishauri Serikali kwamba isijitoe katika suala zima la uwekezaji wa viwanda na naomba Serikali isitegemee wawekezaji kutoka nje peke yao. Ni lazima Serikali ijipange kuhakikisha tunawawezesha Watanzania wa kati, wafanyabishara wadogo na wafanyabiashara wakubwa ili wawe na uwezo wa kujenga viwanda hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo viwanda peke yake, ni pamoja na kilimo na hasa Mwenyekiti hapa ninaposisitiza, uchumi wetu hauwezi kukua kama kilimo chetu bado ni cha kutegemea mvua. Nahimiza twende na kilimo cha umwagiliaji na tuongeze wigo, badala ya kutegemea mikoa ya Nyanda za Kaskazini ndiyo zilishe nchi nzima, hebu tuangalie na Kanda ya Ziwa iliyozungukwa na mito na maziwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuangalie mikoa ya Kanda ya Kati ambayo bahati mbaya ni mikoa kame, kuna Mkoa wa Tabora, Singida, Dodoma ambapo sasa hivi mvua zinanyesha mpaka tunakosa pa kupita, lakini Mkoa wa Dodoma kila siku wanalia njaa na tunategemea Mkoa wa Ruvuma na Rukwa. Naiomba Serikali iipe sekta ya kilimo fursa ya pekee na katika bajeti inayokuja tuipe nafasi inayostahili, tuipe fedha ya kutosha ili sekta ya kilimo iweze kuleta tija. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri ili tuweze kufikia malengo tunayokusudia, ni lazima tujielekeze katika suala la uvuvi na tujielekeze katika kuvua katika kina cha bahari kuu. Tujenge Bandari na hasa hiyo ya Bagamoyo na Bandari zingine. Kama hatutaweza kwenda kuvua kwenye kina cha maji marefu, tukaifanya sekta ya uvuvi kama ni sekta ya uzalishaji ya kiuchumi, Mpango wetu utabaki kuwa kwenye makaratasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pia, hebu watumie ushauri aliotoa Mwenyekiti Chenge na timu yake wakati ule wa bajeti, Waziri wa Fedha, achukue ushauri ule, ni ushauri mzuri sana, kuna mambo mengi sana yapo mle, hebu angalieni vyanzo vipya ili uchumi wa nchi yetu uweze kukua na tuweze kupiga hatua mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali yetu, pamoja na mipango mizuri iliyowekwa hapa, lakini tujielekeze katika kuwawezesha wanawake kiuchumi. Nimefurahishwa na Mpango uliopo wa kupeleka milioni 50 katika kila kijiji na mtaa, naomba katika mpango unaokuja, lazima tuweke mfumo, hizi milioni 50 zitafikaje katika kila kijiji…
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nikushukuru wewe na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu kwa ustawi wa Taifa ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Joyce Lazaro Ndalichako na timu yake yote kwa kuandaa na kuwasilisha vizuri sana hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya fedha kwa mwaka 2016/2017. Pia natoa pole kwa Naibu Waziri Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya kwa kuondokewa na mzazi wake mpendwa. Naomba Mwenyezi Mungu ampe moyo wa uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo na roho ya marehemu iwekwe mahali pema peponi. Amina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa mchango wangu kwenye makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya elimu, sayansi, teknolojia na ufundi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ubora wa vitabu vinavyotumika kufundisha mashuleni, wakati soko huria la utengenezaji na usambazaji wa vitabu likilenga kupunguza uhaba wa vitabu Serikali idhibiti ubora wa vitabu ili kuhakikisha vitabu vinavyotumika shuleni vinakuwa na ubora ili kuzalisha wasomi wazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa nini kifanyike kwenye mtaala wa elimu, Serikali kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu itengeneze mfumo ambao vijana wengi watakwenda kwenye Vyuo vya Ufundi na hivyo kuwa na wazalishaji wengi ambao wataweza kuunda vitu mbalimbali na sio kuwa na kundi kubwa la wasomi wa vyuo vikuu ambao watakuwa wanatafuta kazi baada ya kutunukiwa shahada zao. Ni muhimu sana Serikali ipitie upya mfumo wetu wa elimu ambao kwa kiasi kikubwa unawaandaa wasomi wetu kuwa waajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano kwa mujibu wa hotuba ya bajeti ya mwaka 2014/2015, idadi ya vyuo iliongezeka kutoka 26 hadi 50 kati ya mwaka 2005 hadi 2014 na hivyo idadi imeongezeka kutoka wanafunzi 40,719 kwa mwaka 2005 hadi wanafunzi 200,986 kwa mwaka 2014. Wasomi wote hawa wanaandaliwa kuwa watawala ambao wataanza kutafuta ajira na hivyo kusababisha nchi kuwa na wasomi wengi ambao watahitaji kuajiriwa na siyo kuwa wazalishaji kutokana na mfumo wetu wa elimu kuwa na nadharia nyingi na siyo vitendo. Katika karne ya sasa ni muhimu Serikali kufanya marekebisho katika mfumo wetu wa elimu ili uwezeshe vijana wetu kuwa wazalishaji pindi tu wanapohitimu elimu ya vyuo vikuu na hivyo kuweza kujiajiri wenyewe badala ya kusubiria ajira za Serikali na mashirika binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na Wizara zake ielekeze pesa nyingi kwenye miradi ya maendeleo na sio kwenye matumizi ya kawaida. Mfano, kwa mujibu wa hotuba ya Wizara ya Maliasili na Utalii iliyosomwa Bungeni na Mheshimiwa Profesa Jumanne Maghembe, kwa mwaka 2015 sekta ya utalii peke yake ilitoa ajira rasmi kwa vijana 500 na ajira 1000 zisizo rasmi.
Aidha, kwa mwaka 2016/2017, Serikali iendelee kuboresha mazingira ya utalii kama vile kununua ndege, kujenga barabara na kujenga viwanja vya ndege ili sekta ya utalii ifanye vizuri ziaidi na hivyo kusaidia kupunguza tatizo la ajira ambalo kwa kiasi kikubwa linatokana na mfumo wetu wa elimu, kuzalisha wasomi wengi wenye shahada ambao wanategemea kuajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika dunia ya sasa Serikali lazima itambue kuwa tatizo la ajira kwa wasomi wetu wa vyuo vikuu linazidi kuongezeka kila siku kutokana na mfumo wetu wa elimu kuwaandaa vijana wetu kuwa waajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwandishi wa kitabu cha Rich Dad Poor Dad Robert Kiyosaki anasema mifumo ya elimu yenye mtazamo wa go to school, study hard, get good grades and find a safe and secure job umepitwa na wakati.
Aidha, mwandishi huyu anashauri mifumo ya elimu ya sasa iwe na mtazamo wa go to school, study hard, get good grades, build your business and become a successful investor. Serikali itazame namna ya kuhakikisha vijana wengi wanapata elimu ya ufundi ambayo itawasaidia vijana wengi kuwa wazalishaji wa moja kwa moja na siyo kutegemea ajira. Katika nchi zilizoendelea kiteknolojia kama China na Japan vifaa vingi vidogo vidogo vinatengenezwa na vijana ambao kwa kiasi kikubwa wana elimu ya ufundi tu. Ingawa tuna vyuo vya ufundi stadi, bado idadi ya wanafunzi wanaojiunga katika vyuo hivi ni ndogo kama ilivyooneshwa katika kitabu cha hotuba ya bajeti ya Wizara ya Elimu, ukurasa wa 95.
Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa vyuo vya ufundi kila mkoa; umefika wakati sasa Serikali ianzishe vyuo vya ufundi kila mkoa ambavyo vitawasaidia vijana wetu kupata elimu ya kuwawezesha kujitegemea na siyo kutegemea kuajiriwa na Serikali. Aidha, vyuo hivi vitoe elimu kutokana na mazingira ya eneo husika. Mfano, vyuo vitakavyojengwa Mikoa ya Iringa, Njombe na Mbeya vitoe elimu ya ufundi juu ya matumizi ya mazao ya mbao na vile vitakavyojengwa katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa vijengwe vyuo vya kutoa elimu ya ufundi na ujuzi na kusindika samaki. Kama Serikali itaweka mfumo ambao vijana wengi watakwenda kwenye vyuo vya ufundi wataweza kuzalisha samani nyingi ambazo Serikali pia inaweza kununua samani ambazo zitakuwa zinazalishwa na vijana wetu hapa hapa nchini kwa matumizi mbalimbali na hivyo kupunguza matumizi ya fedha za kigeni kutokana na kununua samani nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais za kujenga Tanzania ya viwanda, ni muhimu vijana wengi wawe na elimu ya ufundi ambao wataanzisha viwanda vidogo vidogo vingi ambavyo vitazalisha samani mbalimbali. Aidha, wasomi wetu wenye elimu ya ufundi wanaweza kuunda viwanda vikubwa ambavyo vitasaidia katika kuleta mapinduzi ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali kwa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi 2016/2017, je, Serikali imejipangaje kwa mwaka 2016/2017 kutatua changamoto za upungufu wa madawati, upungufu wa nyumba za Walimu na madai ya Walimu ambayo ni muhimu hasa katika kuimarisha sekta ya elimu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kifanyike kwa mwaka 2016/2017, katika Wizara hii, baada ya Serikali ya Awamu ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli imeanza kutoa elimu bure na hivyo watoto wengi wamejitokeza shuleni na hivyo kusababisha shule kufurika watoto wengi. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili, Wizara ya Elimu na wadau mbalimbali wa maendeleo waweke mpango mkakati wa kutatua changamoto hizi kama vile kushawishi wananchi, taasisi binafsi na Serikali katika kuchangia ununuzi wa madawati na ujenzi wa vyumba vya madarasa ili kuwezesha watoto wengi kupata elimu.
Aidha, kwa mwaka 2016/2017, Serikali iendelee kuboresha mazingira ya kazi na makazi ya Walimu hasa wale walioko vijijini. Walimu wapandishwe madaraja na kulipwa stahili zao bila kucheleweshewa, pia kwa mwaka 2016/2017, Serikali ianze kuwapa motisha ili kuwapa moyo na kuwahamasisha wengine kufanya kazi kwa bidii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu za kuunga mkono makadirio ya mapato na matumizi Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi 2016/2017 yapitishwe, katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Wizara imeomba kupitishiwa jumla ya shilingi trilioni 1.396 huku matumizi ya kawaida yakiwa ni shilingi bilioni 499 sawa na 35.7% ya bajeti yote huku miradi ya maendeleo ikitengewa shilingi bilioni 897 sawa na 69.1%. Ili kuunga mkono jitihada za kuinua kiwango cha elimu kwa mwaka 2016/2017, Serikali imedhamiria kuinua kiwango cha elimu kwani kati ya shilingi bilioni 897, Serikali imetoa shilingi bilioni 620 sawa na 69.1%, ni fedha za ndani huku 30.9% ikiwa ni fedha za nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2016/2017, Serikali ihakikishe kuwa fedha zilizotengwa kwa ajili ya Wizara ya Elimu zinapelekwa kwa wakati ili kuimarisha kiwango cha elimu nchini. Mfano wa mwaka 2015/2016 hadi tarehe 30 Aprili, 2016 Serikali ilipeleka shilingi bilioni 789 sawa na 72.12% ya bajeti yote. Kwa sababu Serikali ya Awamu ya Tano imejiimarisha katika ukusanyaji wa mapato yanayotokana na kodi ni vizuri kwa mwaka 2016/2017 Serikali ipeleke fedha za miradi ya maendeleo kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuinua kiwango cha elimu, Serikali imeongeza kiwango cha bajeti kutoka shilingi trilioni 1.094 hadi shilingi trilioni 1.396 sawa na ongezeko la 21.6% kutoka mwaka 2015/2016 hadi 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu katika hoja hizi mbili ambazo zipo mbele yetu za Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Utumishi wa Umma.
Awali ya yote napenda nichukue nafasi hii, kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mungu muweza wa yote, aliyenipa nafasi kuweza kusimama na kutoa mchango wangu katika Bunge lako hili Tukufu. Naomba nianze kabisa kwanza kumpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya ya kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kwa kiwango cha hali ya juu sana.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nichukue nafasi hii kumpongeza Rais kwa masuala machache yafuatayo:-
Nitaanza kusema kwamba, nianze kumpongeza Rais kwa jinsi alivyounda hizi Wizara mbili, Wizara ya TAMISEMI na Wizara ya Utumishi na jinsi alivyozipanga na kuhakikisha Wizara hizi zinakuwa chini yake, nimpongeze kwa kuwachagua Mawaziri mahiri, Mheshimiwa Angellah Kairuki, na mwenzake Mheshimiwa Simbachawene. Hakika Mawaziri hawa wana weledi mkubwa, wanafanya kazi kwa uaminifu mkubwa, ni watendaji ambao ni wachapakazi na kwa kweli tuna imani nao. Ukweli umedhihirisha jinsi walivyoandaa hotuba zao, na jinsi ambavyo wameziwasilisha kwa kwelie napenda nichukue nafasi hii kuwapongeza.
Vilevile nimpongeze Rais kwa jinsi alivyoanza, kuhakikisha anapunguza na kumaliza tatizo kubwa sana sugu la mishahara hewa katika nchi yetu ya Tanzania. Ni ukweli usiopingika mara tu baada ya Rais kuchagua Wakuu wa Mikoa aliwapa siku 19 wahakikishe wanabaini watumishi hewa, lengo likiwa ni kuhakikisha fedha zilizokwenda kwenye mishahara hewa ziweze kwenda kwa wananchi.
Naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais, kipekee niwapongeze sana Wakuu wa Mikoa kwa kazi njema wanayoendelea kuifanya kuhakikisha wanabaini wafanyakazi wote hewa ili fedha itakayokuwepo iweze kwenda kwenye miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Rais jinsi anavyobana matumizi, katika uendeshaji wa Serikali, ni ukweli usiopingika kwanza amechagua Baraza dogo, vilevile hata yale matumizi yasiyokuwa na tija Mheshimiwa Rais ameyabana, ninaomba aendelee kufanya hivyo ili kuhakikisha fedha zile ambazo zilikuwa zinatumika katika matumizi ya kawaida ziweze kuelekezwa kwa wananchi na hasa katika masuala mazima ya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Mheshimiwa Rais kwa kweli kwa utendaji wake bora, amesimamia nidhamu ya watumishi na uwajibikaji katika Serikali yake aliyoiunda. Ni ukweli usiopingika tangu ameingia madarakani wafanyakazi wote nchini wameonesha uwezo mkubwa kufanya kazi kwa kuwajibika, wanawahi kazini, wameendelea kuwa waaminifu, wanafanya kazi kufa na kupona ili kuhakikisha dhamira ya Mheshimiwa Rais inakutekelezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kusema wale wote wanaobeza juhudi za Rais naomba Watanzania tuwapuuze kwa sababu ndiyo kawaida yao, maana kila siku wanaamka na jipya, tulipokuwa kwenye Serikali ya Awamu ya Nne walisema Serikali hii siyo sikivu, Serikali imechoka, Serikali ina watu wapole sana; amekuja Dkt. John Magufuli, ameanza kazi leo wameanza kulalamika. Naomba wananchi muwapuuze na Dkt. John Pombe Magufuli endelea kuchapa kazi, akina mama na Watanzania tuko nyuma yako na ninapenda kuwathibitishia Watanzania na Wabunge wenzangu kwamba kabla ya kuja hapa nimetembea zaidi ya Mikoa tisa wananchi wanasema kama kura zingepigwa leo ushindi wa CCM kwa nafasi ya Rais, Wabunge na Madiwani ungekuwa zaidi ya asilimia 100. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanasema, hata wale ambao hawakumchagua Mheshimiwa Magufuli, wanatamani uchaguzi ungerudiwa leo na hata wale ambao hawakumchagua wanajuta, wanasema turudie uchaguzi leo ili wampigie kura zote Dkt. John Pombe Magufuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane na Dkt. Rweikiza alisema ukiona kule watu wanaanza, ukiona wanafanya jambo halafu wapinzani wanapiga kelele umewabana pabaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Dkt. Magufuli endelea tuko nyuma yako na nakuomba endelea kutumbua majipu na hata yale yaliyosababisha mishahara hewa na mengine yako humu ndani na ndiyo maana mengine yalikimbia ili nchi yetu ipate tija, kwa maendeleo yetu...
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mara baada ya kusema hayo napenda niendelee kumwomba Mheshimiwa Rais asisikilize porojo na propaganda zozote kwa sababu suala zima la mihemko huwa lina wakati wake na mihemko ina mwisho wake.
TAARIFA...
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa nimeipokea na huo ndiyo ukweli, wataisoma namba, mara baada ya uchaguzi huo sasa...
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya utangulizi huo naomba nijielekeze kutoa mchango wangu katika maeneo machache ambayo nimeyachagua na kuyatilia mkazo kama ifuatavyo; pamoja na kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi ya kupeleka fedha kwa ajili ya mifuko ya wanawake na vijana asilimia kumi kwa ajili ya vijana na wanawake, na mkakati uliopo kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi, wa kupeleka shilingi milioni 50 katika kila mtaa na kila kijiji, naomba kutoa ushauri ufuatao:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kupeleka asilimi kumi ya vijana na wanawake, kwenye baadhi ya Halmashauri imekuwa ni kitendawili, bado kuna baadhi ya Halmashauri hapa nchini na Manispaa na Miji na Majiji agizo hili hawalitekelezi kikamilifu, ombi langu nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama hapa mbele yetu, atuambie hivi suala la kupeleka asilimia kumi kwa ajili ya vijana na wanawake ni la hiari, ni la kisheria, ni la utaratibu gani, na kama ni la kisheria ni kwa nini Halmashauri, Manispaa na Majiji hawatengi fedha kama ilivyokusudiwa na Serikali yetu? Nitapenda Mheshimiwa Waziri atakapokuwa akihitimisha hotuba yake, atuambie kama jambo hili siyo la kisheria, je, yeye kama Waziri ambaye ameaminiwa na Mheshimiwa Rais ana mkakati gani kuhakikisha, anaileta hii sheria hapa Bungeni ili tuweze kutunga hiyo sheria itakazozibana Halmashauri, Majiji na Miji ambayo hawatengi asilimia kumi ya vijana na wanawake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu wanawake wa vijijini, wanawake wa mijini, wanavikundi vya VICOBA, wanavikundi vya ujasiriamali, wana SACCOS lakini Halmashauri zetu na Miji yetu bado wanafanya mzaha katika kupeleka fedha zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali, katika ule mkakati wa kutekeleza Ilani ya CCM ya kupeleka shilingi milioni 50 kila kijiji na shilingi milioni 50 kila mtaa, naomba kabla ya Bunge hili halijaisha tunataka kuona fedha hizo, nataka tuone fedha hizo hata kama zinapitia kwenye Serikali za Mitaa, hata kama zitapitia Benki ya Wanawake, hata kama zitapitia Benki ya NMB, hata kama zitapitia kwa Wizara yenyewe ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, hata kama zitapitia kwenye Mfuko wa Vijana, tunaomba fedha hizi, kabla ya Bunge hili halijafungwa, Waziri wa Fedha aje hapa mbele yetu atuambie fedha hizi ziko wapi, tuziangalie katika kitabu hiki ziko wapi, na zianze kupelekwa vijijini kama ambavyo zimekusudiwa ili wanawake na vijana wa Tanzania waweze kunufaika na mpango huu wa Chama cha Mapinduzi kwa sababu Chama cha Mapinduzi kimedhamiria kuwaondoa katika umaskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika masuala mazima ya maslahi ya wafanyakazi. Wafanyakazi wa Tanzania, wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana ya utendaji kazi katika nchi yetu, hata haya matunda tunayoyaona mazuri ya utekelezaji wa ilani ya CCM, wafanyakazi wa Tanzania wana mchango mkubwa. Ombi langu katika kupeleka mishahara ya wafanyakazi, ile Bodi ya Tume ya Mishahara iangalie uwiano, tusipishane sana, unakuta Mbunge anapata mara mbili, unakuta kiongozi wa shirika anapata mara tatu, lakini huyu karani, huyu dereva, huyu askari polisi, huyu nesi, huyu daktari, tufanye uwiano ili mishahara na hao wafanyakazi wa kawaida wanaofanya kazi zilizo sawa, waweze kutendewa haki maana kwa kweli ndiyo tegemeo letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la wafanyakazi, kuna nyumba za wafanyakazi, kuna maslahi yao na hasa wanaoishi vijijini walimu wetu, manesi, madaktari, askari…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, mengine nitayaleta kwa maandishi, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kutoa mchango wangu katika hoja iliyo mbele yetu, hoja ya Bajeti ya Serikali ya mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru sana wewe na kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote aliyenipa nafasi ya kuweza kusimama na kuweza kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu iliyo mbele yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nianze kuungana na Wabunge wenzangu wote kukupongeza sana wewe Naibu Spika kwa kazi nzuri unayoifanya ya kuendesha Bunge letu Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa weledi na uwezo mkubwa sana wa kiwango cha kupigiwa mfano. Hakika Dkt. Tulia ni kijana mdogo, ni mara yako ya kwanza kuwa Naibu Spika na ni mama ambaye kwa muda mfupi umetushangaza wanawake, umewashangaza Watanzania na umeshangaza hata ulimwengu kwa jinsi ulivyo mwaminifu, mvumilivu na siyo hivyo tu na jinsi unavyojua Kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, umetukumbusha mpaka enzi za Mzee Mkwawa na Maspika waliopita. Una muda mfupi ndani ya Bunge, umepitia Hansard kwa muda mfupi na kila unaporejea Kanuni pia unarejea Hansard na unatoa mifano ya Maspika wenzako. Kwa kweli, wale wanaokubeza nakuambia lala usingizi, wanawake tupo nyuma yako na tumejiandaa kikamilifu, wameanza wao tutamalizia sisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema hatuna muda wa kupoteza, mara baada ya Bunge Tukufu kukamilisha kazi zake utatusikia na huko tutakwenda kuongea na wananchi kwa sababu uwezo tunao. Dkt. Tulia tutakutetea, chapa kazi na tupo nyuma yako maana kama ingekuwa ni adhabu wangempa Mzee Chenge ambaye yeye ndiye aliyewatoa leo iweje wanakususia wewe ambaye umesimamia Kanuni na taratibu za Bunge! Hongera sana Dkt. Tulia, songa mbele, tupo nyuma yako, Watanzania na wananchi wenye weledi wanakuunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waswahili wanasema ukiona baadhi ya wanaume anapokalia mwanamke kiti wanakimbia, nafikiri hapo jibu lao mnalo, maana mwanaume hakimbii boma. CCM oyee, aah, sorry. (Makofi/Kicheko) [Maneno haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]
Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya utangulizi huo, nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja hii ya bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 kwa asilimia 100 na sababu ninazo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya kwanza ya kuunga mkono, Mheshimiwa Waziri na timu yake yote imeandaa bajeti hii kwa weledi wa hali ya juu sana. Bajeti hii kwa kweli imekonga moyo wangu na imekonga mioyo ya Watanzania kwa sababu ni bajeti inayokwenda kujibu matatizo ya wananchi, inakwenda kujibu kero za wananchi, inakwenda kuwapa wananchi fursa mbalimbali katika utekelezaji wa Ilani ya CCM, inakwenda kutekelezwa kwa kuhakikisha inaweka nidhamu ya uwajibikaji ndani ya watumishi wa umma na siyo kwa watumishi wa umma peke yake na hata wananchi na inakwenda pia kutekeleza maandiko ya Vitabu Vitakatifu ambavyo vinasema asiyefanya kazi na asile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa Fedha na timu yake kwa sababu bajeti hii pia inakwenda kuondoa kodi zote ambazo zilikuwa ni kero kwa wananchi. Mfano, bajeti hii inakwenda sasa kuondoa kodi ya madawa ya maji, mimi kama mama ni jambo ambalo nimelizungumza. Katika miaka mitano nilikuwa kwenye Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji, Kamati ile ilipiga kelele kwa miaka mitano haikufanikiwa lakini bajeti hii inakuja na pendekezo la sisi Wabunge kwenda kuondoa kodi ya madawa ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii inakuja na pendekezo la kuondoa ushuru na kodi katika mazao ya kunde ikiwemo maharage ya soya, karanga na siyo hivyo tu, mboga mboga na hata mazao mengine ambayo yanakwenda sasa kuimarisha lishe ya Watanzania na hasa kwa kuzingatia kwamba kwa mujibu wa tafiti zilizofanyika inaonesha bado Tanzania na hasa watoto na wanawake wanaojifungua wana utapiamlo. Kwa hiyo, kupitia bajeti hii pia inakwenda kuwakomboa wanawake na watoto kwa sababu imeondoa kero ambazo ni sumbufu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya utangulizi huo nijielekeze katika mambo ambayo nimechagua kuyazungumzia ambayo ni machache kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nimefurahishwa na kufutwa misamaha ya kodi ambayo haileti tija kwa wananchi na moja ya jambo hili ni kwenda kufuta misamaha ya kodi katika maduka ya majeshi na maduka mengine katika taasisi zetu za kijeshi. Namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up hapa asituambie kwamba atakwenda kushauriana na viongozi wa wakuu wa majeshi, no! Namuomba na kumshauri aje kabisa na mpango mzima utakavyokuwa, kama inawekwa posho kwa ajili ya hawa askari wetu ijulikane, kama ni shilingi laki moja kwa mwezi ijulikane, ni shilingi laki moja na hamsini ijulikane. Maana akisema anakwenda kushauriana nao endapo watasema ni shilingi laki tatu ataipata kupitia bajeti ipi? Ina maana itakuwa ni mwaka mwingine wa fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza hivyo kwa sababu askari wa nchi hii wamenituma, ma-CP, ma-WP ma-Constable huwa naongea nao sana, wanataka Serikali itoe kauli leo kwamba inakwenda kufanyaje sasa kwa sababu ushuru umeondolewa katika maduka yale ambayo yalikuwa ni msaada kwao. Serikali iweke kabisa fedha kama ni shilingi laki moja na hamsini kama ni shilingi laki tatu kwa kila mwezi ijulikane badala ya kwenda kufanya mazungumzo na viongozi wa jeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu nyingine ni suala zima la kupeleka fedha kwa Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali. Naomba niungane na wenzangu wote walioiomba Serikali yetu Tukufu ambayo ni sikuvu kuongeza fedha, shilingi bilioni 47 kwa ajili ya CAG haitoshi! Kwa bahati njema katika Bunge hili umenipa fursa ya kuwa Mjumbe wa Kamati ya LAAC kwa muda mfupi tumekagua Halmashauri 30 hazikufanya vizuri, tumejionea madudu! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za miradi ya maendeleo zinaliwa sana kwenye baadhi ya Halmashauri zetu lakini Mkaguzi wa Hesabu za Serikali ndiye anayetuletea taarifa. Wenzangu wameshafanya uchambuzi sitapenda kurudia, ili TAKUKURU aweze kufanya kazi yake vizuri lazima na huyu CAG tumpe fedha ili ziende kutekeleza kazi ambayo tumekusudia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, waliposikia kwamba CAG hana fedha baadhi ya Wakurugenzi wasio waaminifu wameanza kushangilia maana wanajua kuna baadhi ya madudu yanafanyika huko hawachukuliwi hatua yoyote, CAG peke yake ndiye atakayetukomboa. Tunamuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha hebu akae na timu yake tena, akaa na timu ya Mama Segasia na wenzake, wajaribu kuona ni wapi wanaweza wakapunguza fedha tukampa huyu CAG ili aweze kufanya kazi yake kikamilifu. Changamoto ya kukosa fedha tumeshaanza kuiona. Mimi niko kwenye Kamati ya LAAC, sasa hivi tunajiandaa kwenda Mikoani, tunajiandaa kuita Halmashauri, unamuona CAG anavyokuja anasuasua maana fedha anazopata hazitoshi. Kama hatumpi fedha za kutosha CAG, tutatenga fedha lakini zitaishia mikononi mwa wajanja kwa sababu watakwenda kufanya sivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumzie utaratibu wa upelekaji wa ujenzi wa miundombinu ya maji katika Serikali yetu. Hapa naomba nianze kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana ambayo imekuwa ikifanya. Tumejionea wenyewe imejenga miradi mikubwa sana ikiwemo jiji la Dar es Salaam na katika miji mingine saba hapa nchini na miradi ya mikakati katika nchi yetu na taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha imeeleza vizuri zaidi na hata taarifa ya Wizara ya Maji. Ombi langu kwa Serikali, kwa sababu zipo shilingi milioni 900 zimetengwa kwa ajili ya maji, tunaomba ule mfuko kwa ajili ya kupeleka maji vijijini uimarishwe, badala ya kutoza Sh.50 kwa kila lita ya mafuta ya diesel na lita 50 ya petrol iwe Sh.100. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu hali ya upatikanaji wa maji na hasa vijijini ni mbaya sana. Mheshimiwa Waziri sijui kama amepata fursa ya kwenda vijijini, mimi ninayezungumza ni mdau wa wanawake na nikienda vijijini sifanyi mikutano ya ndani naitisha mikutano ya hadhara. Hivi navyozungumza nimetoka site siongei mambo ya mezani. Napoitisha mikutano ya hadhara kuongea na wananchi ukiuliza kero ya kwanza kwa wananchi wote, wanawake, wanaume, vijana na watoto ni maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa jinsi alivyoanza kazi vizuri hebu sasa huu Mfuko wa Maji akubali uongezwe tozo kutoka Sh.50 mpaka Sh.100 kwa kila lita ya diesel na lita ya petrol. Ushauri huu unakuja sasa mara ya pili, Wizara ya Fedha kuna kigugumizi gani cha kufanya uamuzi? Mnahofia kwamba eti mkipandisha hapa wananchi watapata matatizo, siyo sawa. Nawaomba sana mshughulikie suala hili kwani kero ya maji ndiyo changamoto ya kwanza. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama na kutoa mchango wangu katika hoja iliyo mbele yetu ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya shukrani hizi, naomba nijielekeze kuchangia. Kwanza, pongezi na shukrani kwa Mheshimwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli. Naomba nianze kwa kumshukuru sana na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa mambo yafuatayo:-
(i) Kwa jinsi alivyounda Wizara hizi nyeti mbili na kuzifanya ziwe chini ya usimamizi wa Ofisi yake na jinsi alivyowateua Mawaziri na Naibu Waziri wenye weledi wa hali ya juu na wenye uchapakazi pia, Mheshimiwa Angellah Kairuki, Mheshimiwa Simbachawene na Mheshimiwa Suleiman Jafo.
(ii) Kwa jinsi alivyoanza kazi na kuhakikisha watumishi wa umma wanakuwa na nidhamu ya kazi, wanakuwa waadilifu na wenye uwajibikaji wa hali ya juu ndani ya Serikali aliyoiunda. Lengo likiwa ni kuleta tija kwa Watanzania wote bila kuleta itikadi za dini, vyama, kabila wala jinsia zao na kuleta maendeleo ya hali ya juu ndani ya muda mfupi na mabadiliko yanaonekana.
(iii) Kwa kubana matumizi katika uendeshaji wa shughuli za Serikali na kutoa zaidi vipaumbele katika miradi ya kuinua uchumi wa nchi.
(iv) Kwa jinsi alivyolipa kipaumbele suala zima la watumishi hewa kwani ameweza kuokoa fedha nyingi ambazo zilikuwa zinapotea bure na kwenda kwa watu wasiohusika wala kuzifanyia kazi. Badala yake fedha hizi hivi sasa zinakwenda kuendeleza miradi mbalimbali hasa kwa wananchi waishio katika kaya maskini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi anayoifanya Mheshimiwa Rais na timu yake ndani ya Serikali imeleta matunda mazuri ndani ya nchi yetu katika muda mfupi kiasi kwamba wale Watanzania ambao hawakumpigia kura wanasikitika sana. Watanzania sasa wanasema itakapofika 2020 hawatafanya makosa tena na CCM kwa nafasi ya Rais, Wabunge na Madiwani watashinda kwa 100%.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, naomba nitoe ushauri katika maeneo machache niliyoyachagua, kwanza, ni uchangiaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Wanawake na Vijana (10%). Pamoja na dhamira njema ya Serikali ya kuzielekeza Mamlaka ya Serikali za Mtaa kutenga 10% kwa ajili ya kusaidia vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana lipo tatizo kubwa la fedha za Mfuko huu kutopelekwa kwa vikundi vya wanawake na vijana kama ilivyokusudiwa kwa sababu halmashauri zilizo nyingi hazitengi kabisa fedha hizi na zinazotenga zinatenga kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa jambo hili linaonekana kama jambo la hiari katika mamlaka husika, napenda kujua, je, utaratibu huu wa kutenga 10% kwa vijana na wanawake upo kwa mujibu wa sheria? Kama ni kwa mujibu wa sheria, je, ni kwa nini halmashauri hazitengi fedha hizi? Je, ni hatua gani zinazochukuliwa dhidi ya watu wasiotenga fedha hizi? Kama utaratibu wa kutenga 10% ya Mfuko wa Vijana na Wanawake hauko kwa mujibu wa sheria, je, ni lini Serikali italeta Muswada huu hapa Bungeni ili tuweze kutunga sheria hiyo itakayowabana wale wote wasiotenga na kufikisha fedha hizo katika vikundi husika?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ucheleweshaji wa fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Utaratibu wa fedha za miradi ya maendeleo katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa zimekuwa ni changamoto kubwa kwani hazitolewi kwa wakati, zinazotolewa ni kidogo na hazitoshelezi kukamilisha miradi na uwiano wa kutoa fedha hizi hauzingatiwi kwani halmashauri zingine zinapata nyingi na zingine kidogo au hakuna kabisa. Napenda Waziri atuambie hapa tatizo ni nini na Serikali ya Awamu ya Tano ina mkakati gani wa kukabiliana na changamoto hizi?
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, upungufu wa wafanyakazi katika mamlaka mbalimbali za Serikali. Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya kupeleka watumishi wa kada mbalimbali katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa, bado lipo tatizo kubwa sana la watumishi katika Halmashauri za Mitaa na hasa Walimu wa sayansi katika shule za sekondari; Madaktari na Wauguzi katika Hospitali za Wilaya, Vituo vya Afya na Zahanati; Maafisa Ugani wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi; na Wakuu wa Idara katika halmashauri nyingi ni wale wanaokaimu. Mheshimiwa Waziri atakapokuwa akihitimisha hoja yake naomba atoe maelezo Serikali imejipangaje kuhakikisha inapeleka wafanyakazi hao katika mamlaka mbalimbali za Serikali ili utendaji wao uweze kuleta tija kwa wananchi?
Mheshimiwa Naibu Spika, nne, maslahi ya wafanyakazi. Pamoja na jitihada zinazoendelea kufanywa na Serikali za kuboresha maslahi ya wafanyakazi bado kuna wafanyakazi wa umma na sekta binafsi wana matatizo ya mikataba; kupata mishahara midogo ya kima cha chini sana; kukosa posho zao za kujikimu au kutopatiwa kwa wakati na makazi yao ni duni sana hasa wale waishio vijijini. Naiomba sana Serikali pamoja na vipaumbele ilivyojiwekea waangalie maslahi ya wafanyakazi hasa Walimu, Wauguzi, Maaskari na wafanyakazi wa halmashauri mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, uimarishaji wa Serikali za Mitaa. Serikali za Mitaa ndiyo sekta pekee inayotoa huduma kwa wananchi siku hadi siku kwa ukaribu zaidi. Ili kuboresha sekta hii nashauri:-
(a) Serikali ithubutu na kufanya uwekezaji ili Mamlaka ya Serikali za Mtaa ziwe na vyanzo vyake vya mapato vya kutosha na kutoa mchango wake katika pato la Taifa;
(b) Mamlaka za Serikali za Mitaa zielekezwe kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuachana na kufanya kazi kwa mazoea, wawe wabunifu ili waongeze wigo wa ukusanyaji wa mapato; na
(c) Serikali za Mitaa kuna upotevu wa fedha kwa matumizi yasiyo na tija na kutozingatia matumizi ya fedha. Kwa hiyo, Serikali lazima ihakikishe kuwa kanuni za fedha zinafuatwa na fedha zitumike kwa malengo yaliyokusudiwa hasa katika kuleta maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niunge mkono hoja na ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.
Lakini vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama na kuweza kuchangia
katika hoja hii muhimu iliyo mbele yetu katika sekta hizi muhimu za miundombinu na nishati.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nianze kwa kukipongeza Chama cha
Mapinduzi kwa kutimiza miaka 40 kwa kuzaliwa kwake kwa mafanikio makubwa sana katika
kuwaletea wananchi maendeleo, ikiwemo miundombinu ya barabara, reli, mawasiliano ya simu
na bandari na kadhalika. Maana ni ukweli usiopingika kwamba kabla ya miaka 40 ya Chama
cha Mapinduzi, hali yetu haikuwa namna hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kukishukuru Chama cha
Mapinduzi na ninaomba kukitakia kila la heri katika miaka mingine 40, kiendelee kutekeleza Ilani
yake na miaka mingine 40 tuwe tumefika mbele zaidi kuliko ilivyo sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nichukue nafasi hii kuwashukuru wananchi wote wa
Tanzania walioshiriki katika uchaguzi wa kata 19 katika chaguzi ndogo za Madiwani na uchaguzi
mdogo wa Jimbo la Dimani ambako Chama cha Mapinduzi kiliibuka mshindi wa kishindo kwa
kupata kata 18 na Jimbo la Dimani Chama cha Mapinduzi kilipata 75%. Kipekee nichukue nafasi
hii kuwashukuru wananchi wa Tanzania na ninaomba niwaambie kwamba imani huzaa imani
na leo tunazungumzia suala la miundombinu ya barabara, tunazungumzia mawasiliano ya simu,
tunazungumzia suala la nishati vijijini, waendelee kuwa na imani na CCM, yote tuliyowaahidi
kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi tutayatekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya utangulizi huo naomba sasa nijielekeze
kwenye mambo machache niliyoyachagua kuyatilia mkazo. Jambo la kwanza naomba
niwakumbushe Wabunge kwamba katika bajeti ya mwaka huu wa fedha 2016/2017 Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha fedha nyingi sana kwa ajili ya maendeleo ya
miradi ya barabara, reli, nishati na kadhalika. Lakini kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa hali
inaonekana kwamba fedha hazipelekwi kwenye miradi kama ilivyokusudiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua nafasi hii kuishauri Serikali, kwa sababu
inabana matumizi katika kuendesha shughuli zake, inakusanya mapato, imebuni vyanzo vipya.
Ninachoiomba Serikali fedha hizo zilizotengwa na Bunge kwa ajili ya miradi ya maendeleo
ninaomba ipelekwe ili miradi iweze kutekelezwa kama ilivyokusudiwa kwa sababu, nimepitia
ripoti za Kamati mbalimbali zilizowasilishwa, Kamati ya Miundombinu kabisa inaonekana hata
30% bado hawajafikia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kutazama Kamati ya Nishati na Madini kiwango
kilichopelekwa ni zaidi ya 25% tu. Ninaiomba Serikali na kwa kweli na Waziri wa Fedha yuko
hapa, hebu tujipange vizuri kupeleka fedha za maendeleo katika miradi iliyokusudiwa kwa
sababu kama haikupelekwa fedha hata kama Mawaziri ni hodari namna gani, hata kama
watendaji ni hodari namna gani hatutafikia lengo lililokusudiwa.
Naomba Serikali ibuni mipango mipya ya kuhakikisha fedha za miradi ya maendeleo
zinapelekwa ili miradi yote iliyokusudiwa iweze kutekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali kuna miradi mingi ya maendeleo ya
miundombinu ya barabara, miundombinu ya reli na miundombinu mingine, na hasa hapa
nizungumzie ya barabara. Kuna miradi mingi iliyoanzishwa mwaka 2010 haikukamilika, 2011
haikukamilika na sasa hivi tuko mwaka 2017 miradi ya baadhi ya barabara haijakamilika na
alipomalizia Mheshimiwa Mipata na hapa nitoe mifano ya barabara za Mkoa wa Mara.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninafurahi sana Waziri wa Miundombinu juzi amekwenda na
amejionea mwenyewe zile barabara hali yake ilivyo, inasikitisha. Barabara ya kutoka Makutano,
Butiama kwa Baba wa Taifa, barabara ya kutoka Butiama kuelekea Mugumu mpaka Loliondo,
mpaka Mto wa Mbu, kwa kweli ni hatari. Ile barabara tangu imeanza kujengwa hakuna
kinachoendelea, Mheshimiwa Waziri amekwenda amejionea kuna wakandarasi wazalendo
zaidi ya 10 wanajenga ile barabara, mimi nimekata tamaa kwa sababu ninachokiona sasa hivi
ni kuchimba tu udongo wanaleta barabarani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ile ni barabara ya kihistoria, ni barabara aliyopita
Baba wa Taifa kudai uhuru wa nchi hii, ni barabara ambayo hatupaswi kupiga kelele namna
hiyo, Mwalimu Nyerere aliangalia Watanzania wote bila kujijali yeye mwenyewe, leo barabara
ya kutoka Butiama kuelekea nyumbani kwake, kwenda Mugumu, kwenda mpaka Loliondo,
kwenda mpaka Arusha ili kufungua barabara wananchi wa Mkoa wa Mara na hasa ukizingatia
kuna mbuga ya wanyama ya Serengeti, kuna ziwa, kuna uchumi uliotukuka, lakini barabara hii
kwa kweli sasa inatuchonganisha kwa wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumejaribu kuzungumza, wananchi wa Mkoa wa Mara wana
imani na CCM, wamechagua CCM, lakini barabara hii sasa inawafanya wanaanza kujenga
wasiwasi.
Ninaomba hatua zichukuliwe, kama Serikali imekuwa ikichukua hatua kwa makandarasi
wabovu, makandarasi ambao wako tayari naomba na hatua zinazostahili huyu mkandarasi
anayejenga hii barabara atazamwe upya, je, anao uwezo? Kwa sababu nimefuatilia fedha
ameshalipwa, ni kwa nini hajengi hii barabara? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sio barabara hii peke yake, barabara zote za ule mkoa haziko
sawasawa. Barabara ya Kisorya - Bunda mpaka hapo Mugumu kupita Nyamuswa mpaka
Serengeti haiendelei! Barabara zote ambazo kwa kweli zimetengewa fedha na zilipitishwa
kuanzia mwaka 2010 hakuna kinachoendelea.
Naomba Serikali hebu ichukue hatua za haraka ili Mkoa wa Mara na wenyewe ufunguke
kwa sababu, ni mkoa wa kiuchumi. Na ukifunguka kuanzia kule Ukerewe mpaka Mara uchumi
wa samaki, uchumi wa madini, uchumi wa mbuga za wanyama na kadhalika. Hata Kaburi la
Baba wa Taifa ni uchumi, maana watalii wanakuja kuangalia kaburi, lakini hawana pa kupita
kwa ajili ya uchumi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumzie suala zima la fedha za Mfuko wa
Barabara (Road Fund). Nimefuatilia kitabu hiki kunaelekea kuna tatizo, hizi fedha pia hazitoki.
Sasa ningependa tutakapokuwa tuna wind up, hebu Waziri atuambie tatizo ni nini? Maana hii
fedha iko kwenye ringfence, hazitakiwi zitoke. Kwa nini haiendi kuhudumia Mifuko ya Barabara
Vijijini, kumetokea kitu gani? Barabara hazipelekewi fedha, barabara zimeharibika tena ni za
vumbi zinazounganisha vijiji na vijiji, kata na kata, lakini hazijengwi kwa Mfuko wa Barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nitoe ushauri, kwa sababu zimekuwa zikitengwa fedha
nyingi na Watanzania wanakatwa kodi kwa ajili ya kuimarisha hizi barabara za vijijini, barabara
zinajengwa na baada ya muda mfupi mvua ikinyesha barabara zinabomoka. Ushauri
ninaoutoa hebu tuangalie sasa mbinu mpya, badala ya kuwa tunajenga barabara za vumbi za
changarawe na kila baada ya mwaka barabara inaondoka na fedha inapotea hebu twende
na mpango mpya sasa wa kujenga hata lami kwa kilometa hata tano, tano. Tunajenga kitu
cha kudumu, kuliko mabilioni ya fedha yanateketea na baada ya muda barabara inaondoka,
halafu sasa tunatenga nyingine kila mwaka. Hebu naomba tubadilike tujaribu kutumia
wataalam wetu wa barabara, hebu watushauri at least tujenge kila kata kilometa tano, tano ili
tuweze kupata matokeo ya haraka na ya mapema. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la upanuzi wa Bandari ya Dar
es Salaam. Nimefurahishwa na maoni ya Kamati yaliyo kwenye ukurasa wa 35 mpaka ukurasa
wa 40. Nayaunga mkono kabisa, na hapa naishauri Serikali na Mamlaka inayohusika, hebu
chukueni ushauri walioutoa Kamati ya Miundombinu muufanyie kazi. Ile gati ya kwanza mpaka
ya saba zipanuliwe, lakini na ile gati ya 13 na yenyewe ijengwe ili Dar es Salaam ipanuke na
meli ziweze kuja za mizigo, zinashusha mzigo kwa haraka na uchumi uweze kukua kwa haraka.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na hapa nishauri, hebu tuangalie na Bandari ya Bagamoyo,
ilikuwa kwenye mpango mzuri na maendeleo yalishafikia hatua nzuri, lakini mimi sioni kama
inazungumzwa na sioni kinachoendelea. Bandari ya Bagamoyo ingejengwa kama ambavyo
tulikusudia na kama ambavyo tuliweka kwenye mpango, nina imani uchumi wa haraka katika
nchi yetu ungeweza kupatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nishauri tujenge na bandari ya Tanga kwa sababu,
Bandari ya Tanga itatuimarisha zaidi maana itawezesha nchi mbalimbali na ikiwemo na Bandari
ya Musoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote, aliyenipa fursa na mimi kuweza kusimama kutoa mchango wangu katika hoja yetu hii iliyo muhimu ya makadirio ya mapato na matumizi ya fedha Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka wa fedha 2017/2018. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuunga mkono hoja na sababu ninazo. Sababu ya kwanza ni kwamba, tangu Serikali imeingia madarakani imefanya kazi kubwa sana yenye kutukuka. Kama kura zingepigwa leo, ushindi wa CCM ungekuwa 99.999%. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kama tutamaliza miaka 10 na Rais huyu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, makofi tuliyompigia juzi Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Wabunge tutasimama juu ya meza kwa kazi anazozifanya. Hongera sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri sana unayoifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa mwaka mmoja Rais umethubutu kutununulia ndege. Ni Bunge hilihili na Wabunge hawahawa walikuwa wanasema na ndiyo maana mimi wakati mwingine huwa nashangaa watu wanakuwa na ndimi mbili; leo wanasema Tanzania haina ndege tunazidiwa na Rwanda, Rais ananunua ndege wanabeza. Waswahili wanasema akutukanaye hakuchagulii tusi na ukiwa kwenye maji unaoga akija mwendawazimu haumkimbizi. Mheshimiwa Rais chapa kazi, tuko pamoja, kazi ni nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais huyuhuyu Mheshimiwa Dkt. John Magufuli amefanya uamuzi wa busara akasema elimu iwe bila malipo kwa watoto wetu. Ni ukweli usiopingika watoto walioandikishwa wamevuka kiwango cha miaka yote iliyopita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais huyuhuyu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, amethubutu. Kwa miaka mingi tangu nchi yetu imeanza, dhamira ya kuhamia Dodoma ilikuwepo, lakini Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ndiyo ameweza.
Hongera sana Rais wetu, chapa kazi, panga Mji wetu wa Dodoma, maendeleo yaendelee na Watanzania wanakuthamini, endelea baba na usiwe na wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais wetu huyuhuyu aliyesikiliza kilio cha Wabunge cha muda mrefu kwamba, mapato mengi ya Tanzania yanapotea, akaziba mianya yote ya upotevu wa mapato. Si Rais mwingine ni Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais huyuhuyu ambaye Wabunge na wengine nawaona wako humu ndani, tulipaza sauti tukasema Rais apunguze safari za kwenda nje ya nchi. Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amepunguza, Wabunge hatuendi nje ya nchi, Rais haendi nje ya nchi,
watumishi tuko humu ndani, gharama za kuendesha Serikali zimepungua. Ni Wabunge ndio tulioshauri ndio maana mimi wakati mwingine nashangaa kuona watu wenye ndimi mbili. Hongera sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri sana unayofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais huyuhuyu ambaye tulimtaka aangalie mishahara hewa. Amedhibiti na leo tunashuhudia jinsi anavyokabiliana na mishahara hewa, wakiwemo watumishi hewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kueleza mafanikio ya Serikali hii ya Awamu ya Tano tutalala hapa. Kama tungeanza kuandika kitabu, Mheshimiwa Rais kwa mwaka huu mmoja ameshafanya mengi ambayo kwa kweli Watanzania na hasa wanawake ambao mimi nawawakilisha, zaidi ya milioni 50 wanawake walioko hapa wamenituma nije kusema wanamshukuru sana Rais, achape kazi na timu yake akiwemo Makamu wa Rais Mheshimiwa Mama Samia, kijana Mheshimiwa Waziri wetu Mkuu, Mheshimiwa Jenista na Baraza lote la Mawaziri na Watendaji wote wa Serikali msirudi nyuma, songeni mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli unabaki palepale ndiyo maana watu sasa wamekosa hoja, tunaanza sasa kuzungumza watu, hatuna cha kusema. Ndiyo maana kila mtu anayesimama anazungumza mtu badala ya kuzungumza maendeleo ya wananchi kwa sababu Mheshimwa Dkt. John Magufuli amefuta na hakuna mtu mwenye swali kwa Serikali ya CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninapoona Wabunge sasa wanaacha kujadili matatizo ya wananchi, binafsi nafurahia kwamba Serikali sasa inasonga mbele, kero zimeisha na ndiyo maana tunaanza kuzungumza mtu mmoja mmoja badala ya kuzungumzia matatizo ya wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee na mchango wangu, nizungumze mambo machache ambayo nimejielekeza kuyachangia kama ifuatavyo.
Taarifa...
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa taarifa nzuri, ndege zinahitaji television. Si jambo baya, ndege zijazo tutakazozinunua miaka ijayo tutaweka television ili Wabunge mfurahie matunda yenu. Mheshimiwa Mwenyekiti, zile nyingine zinazokuja tutaweka television mtembee raha mustarehe kwa sababu Mheshimiwa Dkt. John Magufuli amedhamiria. Ahsante sana kwa taarifa nzuri. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ndio maana mimi nasema watu wenye ndimi mbili. Ni Mheshimiwa Kikwete huyuhuyu walisema alikuwa hafanyi kitu, leo hapa mtu anasema haya yalifanywa na Mheshimiwa Kikwete. Ahsante sana kwa kutambua kwamba na Mheshimiwa Kikwete alitoa hayo mawazo ya elimu bure. Ahsante Mheshimiwa Waitara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze katika mambo matatu ambayo nimeyapanga kuyatilia mkazo. La kwanza, nimejipanga kuelezea uwezeshaji wa wananchi na la pili, masuala ya maji, sekta ya afya na kama muda utaniruhusu nitazungumzia kidogo elimu na kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 15 - 17 Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza kwa kina jinsi ambavyo Serikali ya CCM ina dhamira nzuri sana ya kuwawezesha wananchi. Hapa naomba nishauri katika maeneo machache ambayo nimeyaona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika kuwawezesha uchumi wanawake na vijana. Naomba nitoe ushauri kwa Serikali, nimejaribu kupekua kwenye hivi vitabu, sijaona ile milioni 50 katika kila kijiji. Ningependa kumwomba Waziri Mkuu, atakapokuja kusimama hapa mbele yetu hebu atuambie hii milioni 50 iko wapi? Maana Bunge lililopita tulipitisha zaidi ya bilioni 50 kwa ajili ya kupeleka kwenye vikundi vya wananchi vya kiuchumi. Napenda Mheshimiwa Waziri Mkuu atakapokuja hapa atuambie ziko wapi na zinatoka lini na utaratibu wa kutoa mikopo hii utakuwa ni nini na wanawake na vijana na wananchi kwa ujumla waweze kushiriki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimepekua katika vitabu vyote ambavyo tumepewa, sijaona ule Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake. Ni ukweli usiopingika kwamba wanawake ndiyo wazalishaji wa Taifa hili, ndiyo nguvu kazi, ndiyo wenye vikundi, ndiyo walezi wa familia, ndiyo
wajasiriamali, lakini kwa bahati mbaya sana ule mfuko ambao ulikuwa ndiyo ukombozi kwa wanawake siuoni katika vitabu hivi. Napenda kumwomba Waziri Mkuu atakapokuja atuambie hivi mpango ni nini katika suala zima la kuwakomboa wanawake? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kama mfuko haujawekwa, hatujachelewa. Bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto itakuja. Turejee Mheshimiwa na Kamati ya Bajeti itusaidie fedha hizi ziingie kwa ajili ya wanawake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni 5% ya Vijana na Wanawake inayotokana na Halmashauri zetu. Kwa bahati njema mimi niko kwenye Kamati ya LAAC, nimejionea kwamba Halmashauri nyingi hazitengi fedha. Nimefanya utafiti nimegundua kwamba hawatengi fedha kwa sababu, hakuna sheria. Wanatekeleza Waraka wa Waziri Mkuu tena wakati ule alikuwa Mheshimiwa Sumaye, ni muda mrefu sana. Naishauri Serikali, hebu ilete sheria hapa Bungeni tutunge sheria itakayoweka masharti ya kutenga fedha hizi kwa ajili ya halmashauri ziende kuwakomboa wanawake na vijana kwa sababu wameanzisha vikundi vingi sana, hawana uwezo wa kufikia vyombo vya fedha na huu mfuko peke yake ndiyo ukombozi kwa wanawake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie masharti ya vyombo vya fedha. Kuna taasisi za FINCA, PRIDE na mabenki mengine wanatoa mikopo, tunawashukuru sana kwa kazi nzuri wanayofanya. Naiomba Serikali iweke riba elekezi kwa sababu baadhi ya taasisi zinatoza riba kuanzia 1% - 35%. Hawa wanawake na vijana wanashindwa kurudisha huo mkopo matokeo yake wananyang’anywa magodoro na vitu vyao vya ndani. Badala ya mkopo kumsaidia yeye unamsaidia yule aliyemkopesha fedha. Hebu Serikali chukueni ushauri wangu, wekeni riba elekezi ili wanawake na vijana waweze kunufaika. (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe na Mwenyezi Mungu muweza wa yote kwa kunipa nafasi ya kusimama na kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu ya mwelekeo wa kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuipongeza Serikali ya CCM kwa kutimiza mwaka mmoja kwa mafanikio makubwa katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ikiwa ni pamoja na Serikali kuhamia Dodoma. Naungana na mpango wa Serikali kuufanya Mji wa Dodoma kuwa mji
wa kisasa uliopangwa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na timu yake kwa kuandaa hotuba nzuri iliyogusa nyanja zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nimejielekeza katika kutoa mchango wangu katika mambo matatu yafuatayo:-
(i) Uwezeshaji wa wanawake kiuchumi;
(ii) Maji; na
(iii) Afya, elimu na kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa15 – 17 wa hotuba ya Waziri Mkuu taarifa inaonyesha jitihada zilizofanywa na Serikali katika kuwezesha wananchi kupitia mipango na programu mbalimbali kwa kuwekeza nguvu zaidi kwa wanawake na vijana na watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupongeza Serikali nina ushauri katika maeneo yafuatayo; wanawake ndio nguvu kazi, wanawake ndio walezi wa familia, unapomkomboa mwanamke kiuchumi unakomboa familia na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu shilingi milioni 50 kwa kila kijiji; katika Mkutano wa Bajeti wa mwaka wa fedha uliopita 2016/2017 Bunge lilipitisha fedha ikiwa ni utekelezaji wa mpango wa kupeleka shilingi milioni 50 kila kijiji katika baadhi ya mikoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua ni kiasi gani cha fedha kilitolewa na kilipelekwa katika mikoa ipi, na ni vikundi vingapi vilikopeshwa vikiwemo vya wanawake na Vijana?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kujua ni kiasi gani cha fedha kimetengwa na ni mikoa gani na mingapi itapelekewa fedha hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ningependa kujua ni mamlaka gani imepewa jukumu la kusimamia mpango wa shilingi milioni 50 kila kijiji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake kutoka Serikali Kuu umekuwa ni mkombozi. Kwa vipindi vya miaka ya hivi karibuni na hata bajeti ya mwaka 2017/2018 mfuko huu haukutengewa fedha, naishauri Serikali itenge na kutoa fedha kwa ajili ya mfuko wa maendeleo ya vikundi vya wanawake kama ilivyofanyika kwa vijana, kutotenga fedha kwa ajili ya wanawake ni kurudisha nyuma jitihada za wanawake katika kujikomboa kiuchumi kwa sababu mfuko huu unaotolewa na Wizara ulikuwa ni ukombozi kwa vikundi vya wanawake badala ya kutengewa asilimia 10 ya mfuko wa wanawake na Halmashauri tu ambao pia hakuna uhakika kwa sababu Halmashauri nyingi hazitengi na kutoa fedha hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo katika Halmashauri kutotenga asilimia 10 kwa ajili ya mfuko wa vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana katika Halmashauri zetu. Naomba kutoa ushauri kwamba kwa kuwa utaratibu wa kutoa fedha hizo asilimia 10 ya vikundi vya wanawake na vijana ni maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu miaka zaidi ya 20 iliyopita, naishauri Serikali kuleta muswada ili Bunge litunge sheria itakayoweka utaratibu wa kutenga, kutoa na kurudisha fedha hizo kwa vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana kuliko ilivyo sasa, kwani jambo la kutoa fedha hizo limebaki kama ni jambo la hisani na si jambo la lazima kwa sababu hakuna sheria inayotekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kila unapofanyika ukaguzi linatokea tatizo la kutotoa fedha vikundi vya wanawake na vijana na katika Halmashauri zilizo nyingi zimeonyesha yapo madeni makubwa. Hapa ningependa kusikia kauli yako Mheshimiwa Waziri Mkuu juu ya ulipaji wa madeni haya ili fedha hizi zielekezwe katika kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, riba katika taasisi zinazotoa mikopo kwa vikundi vya wanawake, vijana na wananchi; pamoja na kuzipongeza taasisi za fedha kwa kutoa mikopo midogo na mikubwa kwa vikundi vya wanawake na vijana. Lipo tatizo katika baadhi ya taasisi za fedha viwango vyao vya riba ni vikubwa sana mpaka kufikia asilimia 35 jambo ambalo husababisha wanawake na vijana kushindwa kujikomboa kiuchumi, badala yake wameambulia kufanya kazi za uzalishaji na kuwanufaisha waliowapa mikopo na wao kuambulia kutaifishiwa mali zao kwa mfano vifaa vya nyumbani kama vitanda, magodoro, vyombo na kuuziwa mashamba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba naiomba Serikali itoe riba elekezi kwa taasisi zote zinazotoa mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana lengo likiwa ni wanawake na vijana wanufaike na mikopo hiyo kuliko ilivyo sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Wanawake ilianzishwa kuwakomboa wanawake waishio vijijini na mijini ambao hawana fursa za kufika taasisi nyingine za fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri, naomba Serikali itoe fedha kwa Benki hii ili ipate mtaji wa kufungua matawi katika mikoa yote hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, masharti ya kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake pia yaangaliwe upya kwa sababu masharti hayatofautiani na masharti ya benki zingine, hivyo wanawake walio wengi hasa waliolengwa na kuanzishwa kwa benki ni wanawake wanyonge ambao hawana mali za kuweka kama dhamana wanashindwa kukopa katika benki hii. Hivyo malengo ya kuanzishwa kwa benki hii bado hayajafikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali irejee upya masharti ya kutoa na kurudisha mikopo ili benki hii ya wanawake iwe ni mkombozi kwa wanawake na Watanzania kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya maji, katika ukurasa 38 – 39 Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza kwa kina jitihada zinazofanywa na Serikali za kujenga miundombinu ya maji. Naipongeza Serikali kwa kazi kubwa ya kujenga miundombinu ya maji katika miji mbalimbali hapa nchini. Pia katika ukurasa wa 38 – 39 taarifa inaonyesha kuwa kufikia mwezi Julai na Desemba, 2016, miradi 90 ya miundombinu ya maji vijijini ilikamilika na kufanya mradi iliyokamilika kuwa 1,301 na kubakia miradi 509.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio yaliyopatikana, suala la maji bado ni tatizo kubwa sana, wanawake bado wanatembea umbali mrefu kwenda kutafuta maji, wanawake bado wameshindwa kushiriki shughuli za kiuchumi kwa sababu wanatumia muda mrefu kwenda kutafuta maji, bado dhamira ya CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwatua wanawake ndoo kichwani bado haijafikiwa kiwango kizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali yafuatayo:-
(a) Kutafuta fedha za kutosha hata kama ni kwa mkopo kwa ajili ya utekelezaji wa miundombinu ya maji hasa vijijini.
(b) Serikali na Bunge likubali kuongeza tozo ya mafuta ya petroli na dizeli kutoka shilingi 50 kila lita ya mafuta hadi shilingi 100 katika kila lita ya mafuta. Fedha zitakazopatikana zielekezwe katika ujenzi wa miundombinu ya maji hasa vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo baadhi ya miradi ya ujenzi wa miundombinu ya maji iliyopangwa kutekelezwa kwa fedha za nje mfano, ujenzi wa mradi wa maji Mwanga, Same hadi Korogwe, ujenzi wa mradi wa maji Mgango, Kiabakari, Butiama, ningepeda kujua fedha za kutekeleza
miradi hii zimekwishapatikana na mradi wa Mwanga, Same na Korogwe upo katika hatua gani? Je, mradi wa Mgango, Kiabakari na Butiama unaanza lini? Kwa sababu mpango wa mradi huu ni wa muda mrefu sana. Mradi wa Muyayango, Sokoni Butiama ni miradi ya muda mrefu lakini mpaka sasa miradi hii ya Mgango, Kiabakari Butiama haijaanza na Mwanga, Same na Korogwe ni wa muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya katika ukurasa wa 39 Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza kazi inayofanywa na Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata afya bora kwa kuboresha miundombinu na upatikanaji wa vifaa tiba pamoja na kuimarisha huduma ya mama na mtoto ili
kupunguza vifo vya wanawake na watoto pamoja na kazi nzuri ya Serikali, naomba kuishauri Serikali kufanya yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuweka mikakati itakayopunguza vifo vya wanawake wanaofariki kwa kujifungua kwa mujibu wa utafiti uliofanyika unaonyesha kuwa kila saa moja mwanamke mmoja anafariki kwa tatizo la kujifungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi vituo vya afya ambavyo havijakamilika Serikali ijitahidi kukamilisha vituo vya afya vilivyojengwa ambavyo havijakamilika. Serikali ijitahidi kutafuta fedha na kukamilisha miundombinu ya vituo hivyo ili viweze kuanza kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa vituo vipya vya afya kila Kata; naishauri Serikali itafute fedha na kujenga vituo vya afya kila mwaka tuwe na vituo vya afya kila Halmashauri za Wilaya vinavyojengwa ikiwa ni hatua muhimu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu; naipongeza Serikali kwa kazi nzuri ya kutoa elimu isiyo na malipo pamoja na pongezi, nashauri Serikali kufanya yafuatayo:-
(i) Kuongeza madarasa katika kila shule ya msingi kwa sababu ongezeko la wanafunzi limeleta tatizo la ukosefu wa madarasa ya kutosha.
(ii) Ujenzi wa mabweni katika shule za sekondari kwa sababu watoto wetu na hasa watoto wa kike wanapata adha kuishi mtaani, kutembea umbali mrefu jambo linasababisha pia mimba za utotoni.
(iii) Kuongeza nyumba za walimu na maslahi ya walimu.
(iv) Upungufu wa walimu wa sayansi, hapa ningependa kujua Serikali kwa sasa ina mkakati gani wa kuongeza walimu hao wa sayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo, nashauri Serikali iongeza wigo kwa kilimo cha umwagiliaji katika maeneo yanayozungukwa na maziwa na mito na maeneo yenye ukame ili kuongeza upatikanaji wa chakula kwa uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama na kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wazee na Watoto. Nianze kwa kuunga mkono hoja na sababu zangu za kuunga mkono hoja ni kama ifuatavyo:-

(i) Randama na hotuba ya Waziri imeandaliwa vizuri na kitaalam; na
(ii) Serikali ya CCM chini ya uongozi wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Waziri mwenye dhamana, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wa Wizara hii wanafanya kazi nzuri ya kuhakikisha wanaboresha huduma za afya hapa nchini. Ni ukweli usiopingika kuwa katika kipindi hiki kifupi, wameendelea kuonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya CCM ya kuboresha huduma za afya kwa wananchi, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi, kwanza napenda kushauri Serikali:-

(a) Itoe fedha za kutosha za utekelezaji wa majukumu ya sekta hii muhimu;

(b) Iboreshe maslahi ya wafanyakazi wa sekta ya afya na maendeleo ya jamii na kuongeza idadi ya wafanyakazi;

(c) Iendelee kununua vifaa tiba katika zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya na mkoa;

(d) Ipeleke wataalam kama vile Madaktari na Wauguzi katika hospitali, vituo vya afya na zahanati zote;

(e) Iandae mpango maalum utakaoleta matokeo ya haraka ya ujenzi wa vituo vya afya, zahanati na ukamilishaji wa mpango wa hospitali za rufaa za kila mkoa, lengo likiwa ni kupunguza msongamano wa wagonjwa katika hospitali za Muhimbili, KCMC na Bugando. Hapa naishauri Serikali kujenga vituo vya afya viwili viwili katika kila halmashauri, kwa halmashauri tulizonazo 183 x 2 x 3 = 1,098;

(f) Ikamilishe vituo vya afya vilivyojengwa kwa nguvu za wananchi ili visaidie kutoa huduma badala ya kubaki kuwa magofu;

(g) Iongeze fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara (Mwalimu Nyerere Memory Center);

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kuongelea huduma ya afya ya uzazi na mtoto. Pamoja na kuipongeza Serikali kwa jitihada zake za kuboresha huduma inayotakiwa kwa wanawake kabla ya ujauzito, wakati wa ujauzito, wakati wa kujifungua na wiki sita baada ya kujifungua, naomba niungane na Serikali katika ukurasa wa 16 kuwa kweli bado ipo changamoto kubwa ya wanawake wanaofariki wakati wa uzazi. Kwa mujibu wa tafiti zilizopo hapa nchini ya mwaka 2015 zinaonesha kwamba vifo vinavyotokana na uzazi havijapungua, idadi ya vifo ni 556 kwa kila vizazi 100,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza mpango wa Wizara ulioandaliwa na unaotekelezwa kuanzia 2016 hadi 2020. Hapa napenda nipate muhtasari juu ya mpango huo, tangu mpango huo umeanza kutekelezwa tumeweza kuokoa vifo vingapi vya wanawake? Ni kwa nini vifo vimeongezeka badala ya kupungua? Takwimu za 2016/2017 zinaonesha hali ikoje juu ya vifo vya wanawake ikilinganishwa na ya mwaka 2015?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, watoto wanaozaliwa kabla ya wakati (njiti). Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Mamaye 2017 kwa kushirikiana DFID, watoto 2,013 wanazaliwa kabla ya wakati na watoto 3,900 waliozaliwa bila kufikisha umri, wanafariki dunia. Watoto wanaozaliwa kabla ya wakati pia ni sababu ya watoto wanaofariki kabla ya kufikisha miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kunusuru maisha ya watoto wanaozaliwa kabla ya wakati naishauri Serikali kufanya yafuatayo:-

(i) Tuwe na wodi/chumba maalum kwa ajili ya watoto hawa kwa sababu hali ilivyo sasa hakuna vyumba maalum katika baadhi ya vituo vya afya na hospitali zetu;

(ii) Kuwe na vitanda vya kutosha kwa ajili ya kuwalaza watoto hao;

(iii) Kuwe na mashine ya kusaidia watoto kupata joto ili kuwafanya waishi;

(iv) Kuwe na mashine za kuondolea ugonjwa wa manjano; na

(v) Elimu kwa jamii itolewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ugonjwa wa saratani – shingo ya kizazi, matiti na tezi dume. Pamoja na kuishukuru Serikali kwa jitihada zake za kupambana na ugonjwa wa saratani kwa kuboresha Taasisi ya Saratani ya Ocean Road na hospitali za kanda ili ziweze kutoa huduma kwa wagonjwa wa saratani, bado ugonjwa wa saratani umekuwa ndio ugonjwa tishio kwa wanawake na wananchi wengine kwa ujumla. Kwa kuwa ugonjwa huu ni hatari na dawa za saratani ni ghali sana, naiomba Serikali itenge na kutoa fedha kwa ajili ya kununua vifaa tiba vya ugonjwa wa saratani. Pia naomba Serikali itoe msamaha wa matibabu kwa wagonjwa wa saratani kama ilivyo kwa wagonjwa wa UKIMWI kwa sababu wanawake na wananchi wanaougua ugonjwa huu wa saratani hawana uwezo wa kumudu kununua dawa za ugonjwa huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, dirisha la wazee, wanawake na wajawazito na watoto chini ya miaka mitano. Pamoja na kupongeza Serikali kwa kuweka na kuanzisha dirisha la wazee na wanawake wajawazito na watoto chini ya miaka mitano, bado ipo changamoto kubwa ya utoaji huduma hii kwa wazee, wanawake wajawazito na watoto. Changamoto kubwa sana ya kundi hili ni dawa/ fedha zinazopelekwa hazitoshelezi. Nashauri, Serikali iwapatie huduma za bima ya afya wazee, wanawake na watoto. Pia iongeze fedha kwa ajili ya kuhudumia kundi hili na kuondoa adha wanayoipata kwa kukosa huduma ya afya kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, uwezeshaji wa wanawake kiuchumi. Wanawake ndiyo nguvu kazi, wanawake ndiyo walezi wa familia, unapomkomboa mwanamke kiuchumi unakomboa familia kwa ujumla. Taarifa inaonesha jitihada zilizofanywa na Serikali katika kuwezesha wanawake kupitia mipango na program mbalimbali kwa kuwekeza nguvu zaidi kwa wanawake na watu wenye ulemavu. Pamoja na kupongeza Serikali, nina ushauri katika maeneo yafuatayo:-

(i) Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake kutoka Serikali Kuu. Mfuko huu umekuwa ni mkombozi. Kwa vipindi vya miaka ya hivi karibuni na hata bajeti ya mwaka 2017/ 2018, mfuko huu haukutengewa fedha. Naomba Serikali itenge na kutoa fedha kwa aili ya Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake kama ilivyofanyika kwa vijana. Kutotenga fedha kwa ajili ya wanawake ni kurudisha nyuma jitihada za wanawake katika kujikomboa kiuchumi kwa sababu mfuko huu unaotolewa na Wizara ulikuwa ni ukombozi kwa vikundi vya wanawake badala ya kutengewa 10% ya Mfuko wa Wanawake na Halmashauri tu ambao pia hakuna uhakika kwa sababu Halmashauri nyingi hazitengi na kutoa fedha hizo.

(ii) Tatizo la kutolipa 10% ya wanawake na vijana. Lipo tatizo katika Halmashauri kutotenga 10% kwa ajili ya mfuko wa vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana katika Halmashauri zetu. Naomba kutoa ushauri kwamba kwa kuwa utaratibu wa kutoa fedha hizo 10% ya vikundi vya wanawake na vijana ni maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu miaka zaidi ya 20 iliyopita, Serikali ilete Muswada ili Bunge litunge sheria itakayoweka utaratibu wa kutenga, kutoa na kurudisha fedha hizo kwa vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana kuliko ilivyo sasa, kwani jambo la kutoa fedha hizo limebaki kama ni jambo la hisani na si jambo la lazima kwa sababu hakuna sheria inayotekelezwa.

Kwa mujibu wa Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kila unapofanyika ukaguzi linatokea tatizo la kutotoa fedha kwa vikundi vya wanawake na vijana, Halmashauri zilizo nyingi zimeonesha yapo madeni makubwa. Hapa ningependa kusikia kauli ya Serikali juu ya ulipaji wa madeni haya ili fedha hizi zielekezwe katika kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana.

(iii) Riba katika taasisi zinazotoa mikopo kwa vikundi vya wanawake. Pamoja na kuzipongeza taasisi za fedha kwa kutoa mikopo midogo na mikubwa kwa vikundi vya wanawake na vijana, lipo tatizo kwa baadhi ya taasisi za fedha viwango vyao vya riba ni vikubwa sana mpaka kufikia 35%. Jambo hili husababisha wanawake na vijana kushindwa kujikomboa kiuchumi badala yake wameambulia kufanya kazi za uzalishaji na kuwanufaisha waliowapa mikopo na wao kuambulia kutaifishiwa mali zao kwa mfano vifaa vya nyumbani kama vitanda, magodoro, vyombo na kuuziwa mashamba. Nashauri Serikali itoe riba elekezi kwa taasisi zote zinazotoa mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana lengo likiwa ni wanawake na vijana wanufaike na mikopo hiyo kuliko ilivyo sasa.

(iv) Benki ya Wanawake ilianzishwa kuwakomboa wanawake waishio vijijini na mijini ambao hawana fursa za kufika taasisi nyingine za fedha. Nashauri Serikali itoe fedha kwa benki hii ili ipate mtaji wa kufungua matawi katika mikoa yote hapa nchini. Vilevile masharti ya kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake yaangaliwe upya kwa sababu hayatofautiani na masharti ya benki zingine, hivyo wanawake walio wengi hasa waliolengwa na kuanzishwa kwa benki ni wanawake wanyonge ambao hawana mali za kuweka kama dhamana wanashindwa kukopa katika benki hii. Hivyo, malengo ya kuanzishwa kwa benki hii bado hayajafikiwa. Pia Serikali irejee upya masharti ya kutoa na kurudisha mikopo ili Benki hii ya Wanawake iwe mkombozi kwa wanawake na Watanzania kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na hizi dakika za Mgimwa najua utanipatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nikushukuru wewe na nimshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote aliyenipa nafasi ya kuweza kusimama na kutoa mchango wangu katika sekta hii muhimu ya Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuunga mkono hoja na sababu zangu ni mbili zifuatazo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, hotuba imeandaliwa vizuri sana, pili, dhamira ya Serikali chini ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri na watendaji wote wa Serikali hasa katika sekta hii ya afya na maendeleo ya jamii kwa kweli wamejipanga. Wanaonesha kabisa dhamira nzuri ya kuhakikisha Watanzania wanakuwa na afya bora. Kwa msingi huo naunga mkono kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nitoe ushauri kwamba kwa kuwa Wizara imejipanga vizuri na kwa sababu changamoto za Wizara ya Afya na changamoto za Wizara ya Maendeleo ya Jamii ni kubwa, nimefurahi leo nimemuona Waziri wa Fedha yupo hapa, ninaomba Serikali ipeleke fedha katika Wizara hii kwa sababu bila afya hakuna kilimo, uchumi wala chochote katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ya Fedha ijitahidi kupeleka fedha kwenye sekta ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, nimejaribu kupitia kitabu hiki kila kitu inaonekana kama taasisi hii hakuna kitu. Taasisi hii ni mtambuka; bila Wizara ya Maendeleo ya Jamii kwa kweli hakuna chochote. Ninafurahi Waziri wa Fedha ananisikiliza na katika mwaka wa fedha ujao tunataka kuona sasa percent inaongezeka katika sekta hii ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri kwa Serikali iboreshe maslahi ya wafanyakazi katika sekta hii. Wanafanya kazi ngumu sana ma-nurse wetu, madaktari na watumishi wetu katika huduma za maendeleo ya jamii, bibi na bwana maendeleo ya jamii, lakini kwa bahati mbaya ni kundi ambalo wakati mwingine linasahaulika.

Nimefurahishwa na hotuba ya Rais juzi wakati wa Mei Mosi kwamba anakwenda kuboreshwa maslahi ya wafanyakazi. Naomba sekta hii ya afya hebu angalieni ma- nurse wetu wanavyofanya kazi kwa tija, angalieni madaktari wetu wanafanya kazi usiku na mchana, wanafanya kazi saa za ziada, hawana kupumzika wala kuchoka lakini zile stahili na posho zao hawazipati kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa Serikali ipeleke vifaa tiba kama ambavyo imeanza kununua dawa, ipeleke vifaa tiba katika vituo vya afya na ipeleke wataalam wa kutosha na hasa kutokana na hili sekeseke lililotokea juzi, watalaam sasa wamepungua katika taasisi zile. Naomba Serikali iwe makini ihakikishe hakuna kituo kinachopungukiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri kwenye ujenzi wa vituo vya afya. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia wanawake wanafariki kwa kukosa huduma, watoto chini ya miaka mitano wanafariki. Ni ukweli usiopingika kwamba vituo vya ya ni vichache, tunaomba Serikali sasa ije na mkakati maalum na hapa naomba nitoe ushauri kwamba sasa Serikali kila Halmashauri tujenge kila mwaka vituo viwili, ukipiga mahesabu kwa Halmashauri tulizonazo 183, kama tutajenga vituo viwili, viwili kila mwaka na inawezekana, tutaweza kufika mbali; mara baada ya miaka mitatu tunaweza kuwa tumejenga vituo zaidi ya 1,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna vituo vya afya vipo ni maboma, vimejengwa hakuna mabaara, havijakamilika, nguvu za wananchi zimeishia pale. Ninaomba sana Wizara ya Fedha hebu tafuteni fedha zozote hata kama ni kwa mkopo, pelekeni ili hivi vituo vianze kwa sababu wananchi wamejikusanya wameishia pale kwa kushirikiana na Wabunge kupitia Mifuko ya Majimbo. Sasa Serikali ni jukumu lake kuhakikisha vituo hivi vinakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii pia iweke utaratibu wa kuhakikisha inaongeza fedha katika maeneo mbalimbali na hasa katika Hospitali yetu ya Mkoa wa Mara. Ameongea Mheshimiwa Bonny Hospitali ya Rufaa ile ya Mkoa Mwalimu Nyerere Memorial Centre ni kituo ambacho kitakuwa ni ukombozi kwa watanzania na hasa wa Kanda ya Ziwa. Bugando sasa imeelemewa, tukipata kituo hiki na Serikali ikipeleka fedha za kutosha kila mwaka badala ya inavyofanya hivi sasa shilingi milioni 200 kila mwaka hakitakwisha leo.

Ninaomba Serikali ikiwezekana ipeleke hela kwa mkupuo shilingi bilioni 10 mwaka mwingine shilingi bilioni 10 ile hospitali ijengwe iwe ni ukombozi kwa hospitali za Kanda ya Ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wanaofariki kabla ya kufikisha miaka mitano. Ninashukuru jitihada za Serikali vifo vimepungua. Kuna tatizo la watoto wanaozaliwa njiti. nimejaribu kupitia kwenye hotuba ya Waziri sikuona eneo hili. Katika vifo vya watoto wanaofariki chini ya umri wa miaka mitano miongoni mwao ni watoto wanaofariki wakiwa njiti ni asilimia 40 na ni sehemu ya pili ya watoto wanaofariki. Ukiangalia takwimu kila siku watoto 100 wanafariki na kila mwaka watoto 9,000...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia. Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote aliyenipa fursa ya kuweza kusimama na kuweza kutoa mchango wangu katika sekta hii muhimu sana ya ardhi ambayo baba wa Taifa aliasisi akasema ili nchi iendelee inahitaji mambo manne na suala la ardhi alilipa kipaumbele cha kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijakwenda kwenye hoja zangu naomba kwanza niseme naunga mkono hoja hii kwa sababu jana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amefanya kazi nzuri sana ya kutukuka ambayo sisi Watanzania na hasa wanawake hatuna cha kumlipa zaidi ya kumwombea kwa Mwenyezi Mungu aendelee kumpa nguvu na kumsimamia aendelee kutekeleza kile alichokiahidi alipokuwa akiomba kura kwa Watanzania na Watanzania wakamwamini na kumpa kura za Urais mpaka 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba kwa kazi aliyofanya Mheshimiwa Rais, maana mimi hapa napokea simu mpaka simu imezima, kama kura zingepigwa leo ushindi wa Chama cha Mapinduzi ungekuwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niunge mkono hoja hii kwa sababu nne zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ya kwanza, kitabu hiki kimeandaliwa vizuri, ni ukweli usiopingika kitabu hiki hakina maneno, kimejeaa data, maneno ni ukurasa 1 – 70 lakini kuanzia ukurasa wa 1 mpaka 157 ni data. Hongera sana Mheshimiwa Waziri Lukuvi na timu yake kwa kuandaa kitabu hiki vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa sababu Mheshimiwa Waziri, William Lukuvi, Mheshimiwa Naibu Waziri, Angelina Mabula; mimi huwa namwita Sanji, na Katibu Mkuu na timu yote wanafanya kazi nzuri sana na ndiyo maana leo naona kila Mbunge anayesimama muda unamtosha kwa sababu hana cha kuzungumza zaidi kwa sababu mambo mengi yamefanyika katika maeneo yake.

Naomba Mheshimiwa Lukuvi aendelee kufanya kazi, pamoja na timu yake na Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa kweli watendaji wa Wizara Ardhi wamebadilika, ameeleza hapo Mheshimiwa Chikota, nimemsikiliza. Siku moja nimewahi kwenda kwenye Wizara fulani tukiwa naye, tulijionea maajabu ambayo yalikuwa hajawahi kutokea; hongereni sana, Mwenyezi Mungu awatie nguvu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naunga mkono hoja hii kwa sababu Wizara ya Ardhi imetatua migogoro mingi sana iliyokuwa inawakabili wananchi kule Dar- es Salaam, Arusha, Mara, Morogoro na maeneo mbalimbali, nikianza kuyataja tutalala hapa kwa upimaji wa ardhi na maeneo mengine; kwa kweli Lukuvi hatuna cha kumlipa; naomba niungane na wenzangu kusema kwamba Mwenyenzi Mungu awatie nguvu na awasimamie katika kila kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada kuunga mkono hoja hii, sasa naomba nijielekeze katika mambo machache niliyojipanga kuyatilia mkazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, nataka nizungumzie umiliki wa ardhi. Napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru Serikali yetu ya CCM kwa kutoa fursa sawa kwa wanawake na wanaume katika kumiliki ardhi. Kwa mujibu wa Sheria ya Mwaka 1979 kifungu cha nne (4) mpaka cha tano (5) kimetoa fursa kwa wananchi wote bila kujali ni mwanamke ama mwanaume kwamba anayo haki ya kumiliki ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi bado yapo matatizo katika jamii ya watu wa Tanzania ambako baadhi ya wanawake hawamiliki ardhi. Kwenye ule utaratibu wa mila baadhi ya makabila mwanamke hamiliki ardhi. Hapa nitatoa mfano wa wajomba zangu kule Kagera ambako mwanamke hana chake, hawezi kumiliki ardhi yeye anamiliki mji tu. Kule Kilimanjaro na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imefika wakati kwamba sasa Mheshimiwa Lukuvi sisi tunakuamini hebu akaangalie taratibu za kimila ambazo ni kandamizi kwa wanawake ili zirekebishwe na wanawake waweze kumiliki ardhi sambamba na wanaume ili wanawake nao wafaidike na matunda ya nchi yao. Wanawake wana fursa, wanawake wana haki ni kwa nini inapofika wakati wa kutoa ardhi eti mila na desturi zinasema wanawake hawana haki? Kwa kweli Mheshimiwa Lukuvi nataka hapa kabla hajahitimisha hotuba atuambie sasa na namwaminia kwa uhodari wake, ana mkakati gani kuhakikisha hizi mila kandamizi zinaweza kuondolewa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie migogoro ya wakulima na wafugaji na vile vile migogoro kati ya wananchi na hifadhi. Sitaki nirudie ya wenzangu waliyozungumza. Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Serikali lakini bado kuna migogoro mikubwa ya ardhi, bado wananchi wanaishi kwa mashaka, bado wafugaji hawana uhakika, bado mazao ya wakulima yanaliwa na mifugo ya wafugaji; bado hifadhi inawakandamiza wananchi; bado hata wananchi wanakwenda kwenye maeneo ya hifadhi ambako hawaruhusiwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ufike wakati sasa na hapa nataka nije na ushauri, umefika wakati Serikali ya Tanzania ipime ardhi yote ya Tanzania. Naomba nikatae kwamba haiwezekani suala la kupima ardhi kuwaachia Halmashauri, Halmashauri hazina fedha. Serikali itengeneze mkakati maalum wa kutafuta fedha hata kama ni kwa mkopo, hata kama ni kuanzisha mfuko na tuko tayari, zitafutwe hela za kutosha, ardhi ya Tanzania ipimwe yote, wakulima waambiwe ninyi eneo lenu ni hili, wafugaji hapa ni kwenu, wavuvi hapa ni kwenu na Hifadhi ya Taifa ni hapa, ili tuweze kuishi kwa amani na utulivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumza wenzangu kwamba sasa hivi population ya Watanzania imeongezeka, idadi ya mifugo imeongezeka lakini ardhi nayo inaendelea kutumika. Kama hatukujipanga na kuwa na matumizi bora ya ardhi huko baadaye kutakuwa na vita vya watu wanaopigania ardhi. Naomba tusifike huko, hebu Serikali ije na mkakati na mpango. Itengeneze mkakati wa kukopa fedha kwenye vyombo vya fedha ili tuweze kupima ardhi yote ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti naomba niipongeze Serikali ya Chama cha Mapinduzi, kwa kazi nzuri sana ya kuendelea kutoa hati kwa Watanzania. Napongeza sasa hivi sekta ya ardhi wameandaa utaratibu mzuri sana, sasa hivi wamefungua ofisi za kanda, ndani ya miezi mitatu mwananchi anapata hati. Zamani ilikuwa ni kero na shida, hongera sana Serikali ya CCM; na ndiyo maana wananchi wanasubiri uchaguzi ufike kwa sababu kazi inafanyika vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri, kwamba pamoja na kazi nzuri, lakini zoezi linasuasua. Tumeona kazi nzuri ya Morogoro tumeona kazi nzuri kule Muleba na maeneo mengine ya kupima ardhi mpaka za vijijini. Sasa hivi naomba nishauri Serikali, hebu iongeze kasi ya kupima ardhi, hebu itafute fedha za kutosha, ipeleke kwenye hicho kifungu ili wananchi wote wapimiwe ardhi yao. Kama mwananchi akipimiwa ardhi yake akawa na hatimiliki hata mapato ya Serikali yataongezeka kwa sababu atalipa mapato kwa mujibu wa Sheria badala ambavyo sasa hivi wananchi zaidi ya asilimia 80 wanatumia ardhi lakini hawalipi chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ardhi itamkomboa wananchi na hasa mwanamke aliye kijijini atatumia hati yake kwenda kukopa fedha katika vyombo vya fedha. Kwa hiyo naomba Mheshimiwa Lukuvi na timu yake na Serikali yote kwa ujumla hebu waweke mkakati wa kuhakikisha tunakwenda kupima ardhi. Hapa nataka atakapo-wind up hotuba yake Mheshimiwa Lukuvi atuambie ana mkakati gani wa kuhakikisha kwamba anaharakisha kwenda kupima ardhi na wananchi wote wanapata hatimiliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la mipango miji. Ukiwa kwenye ndege ndio utaona hali halisi. Ukienda nchi nyingine utaona ardhi imepimwa vizuri. Afrika Kusini ni mfano na maeneo mengine, kwetu unaona viduku viduku vimekaa. Ufike wakati sasa tuwe na mipango miji, tuwe na master plan ya kila mji. Tumechoka kuona miji yetu inajengwa bila kuwa na master plan. Sasa hivi tunaanzisha Jiji la Dodoma, Makao Makuu ya Chama na Serikali, tunataka Mji wa Dodoma upimwe wote, tunataka mikoa mipya na mikoa mingine ipimwe yote na maeneo yote ya halmashauri na miji yetu ili tuwe na miji iliyopangwa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile niipongeze National Housing kwa kazi sana wanayoifanya ya kujenga nyumba. Hongera Mr. Mchechu na timu yako, mmekuwa ni watu waaminifu na waadilifu, mmefanya kazi nzuri sana iliyotukuka ya kujenga nyumba za National Housing hapa Tanzania; lakini kama alivyosema Mheshimiwa Lupembe nyumba nyingine hazina watu, tatizo linalowapata nyumba ni ghali. Tunaomba mjaribu kufanya marekebisho. Tafuteni sasa, mkawasaidie na wanyonge hasa wanawake wanaoishi vijijini. Huyu mfanyakazi mdogo mwenye kima cha chini mshahara wake shilingi laki mbili ama laki tatu naye afaidike na mpango huu na inawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mr. Mchechu namfahamu, huwa ana mipango; anaweza akatengeneza hata nyumba ya milioni kumi mtu akaishi, anaweza kutengeneza nyumba ya milioni ishirini mwananchi akaishi; ikiwezekana hata ya milioni tano, chumba na sebule ataishi mfanyakazi wa Tanzania na akafaidika kuliko ilivyo sasa milioni mia moja na nyumba ya kima cha chini milioni arobaini kwa kweli inashindikana. Siyo National Housing peke yenu hata na ile kampuni ya Watumishi Housing pia nao wamefanya nzuri lakini warekebishe hivi viwango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nipongeze sana mpango wa mashine za kufyatulia matofali kwa vijana, naomba sasa National Housing, Mr. Mchechu na wenzake waje sasa na mpango wa kusaidia wanawake. Wanawake nao wanao uwezo wa kufyatua matofali kwa ajili ya kujenga nyumba za bei nafuu, nao wakopesheni kupitia vikundi vyao ili nao wanufaike na mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, mchango wangu mwingine nitauwasilisha kwa maandishi, naunga mkono hoja, hongera sana Waziri wa Ardhi, hongera sana Mheshimiwa Dkt.Magufuli Mungu akubariki sana kura zikipigwa leo Rais ni wewe. Ahsante sana Kidumu cha Chama cha Mapinduzi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuungana na wenzangu kuweza kuchangia katika hoja hizi mbili Ofisi ya TAMISEMI na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote aliyenipa fursa ya kuweza kusisimama na kuweza kuchangia katika Bunge lako Tukufu. Nitoe pole sana kwa wananchi wenzetu Afrika Kusini kwa kuondokewa na muasisi wetu mama Winnie Mandela. Naomba niungane nao sisi Chama cha Mapinduzi tumepeleka mwakilishi na UWT tumepeleka mwakilishi, tunaomba tuungane nao na Mwenyezi Mungu ampoke na amlaze mahala pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na timu yake yote ya Serikali yake kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya ya kutekeleza Ilani ya CCM kiasi kwamba hata tukifanya uchaguzi hata hizi ndogo zilizopita Chama cha Mapinduzi kinaibuka na ushindi mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni dalili tosha kwamba hata kura zingepigwa leo za Mheshimiwa Rais na hata kura zingepigwa leo za Wheshimiwa Wabunge na hata kura zingepigwa leo za Serikali za Mitaa na hata Madiwani Chama cha Mapinduzi kingepata ushindi wa asilimia 100 kwa sababu wananchi wana imani nacho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumtia moyo Mheshimiwa Rais kuwatia moyo Waheshimiwa Mawaziri wote na hasa TAMISEMI na Utumishi waendelee kuchapa kazi na sisi wanawake wa Tanzania tuko nyuma yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya utangulizi huo, naomba sasa nijielekeze katika mambo machache niliyoyachagua kuyatilia mkazo. Hapa nitaanza na kwa kweli kuipongeza Ofisi ya TAMISEMI chini ya kijana wetu shupavu Mheshimiwa Jafo kwa kazi nzuri sana waliofanya ya kudhibiti matumizi ya fedha na mapato yake. Kwa mujibu wa taarifa ya mkaguzi wa hesabu za Serikali inaonesha kwamba kwa halmashauri zilizokaguliwa 166 halmashauri zimepata hati safi zaidi asilimia 90. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni mkombozi mkubwa sana kwa sababu nilikuwa mjumbe wa Kamati ya LAAC tulikuwa tukiona madudu mengi katika halmashauri, matumizi ya fedha yalikuwa ni ya ovyo, watu walikuwa hawafuati kanuni za fedha, fedha zilikuwa zinaibiwa, lakini kwa usimamizi wa Mheshimiwa Waziri na wenzake kuwa makini naona sasa matokeo mazuri yanakuja. Ni matumaini yangu sasa hata fedha zitakazokaguliwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018 tutapata asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze mpango wa kukusanya mapato ni ukweli usiopingika kiwango kimeongezeka, lakini niseme ukweli bado hakijawa cha kuridhisha. Ni asilimia 50 tu ya mapato yote yaliyokusanywa katika halmashauri, lakini unasikiliza huku Wakurugenzi kilio kingi wanazungumzia sijui mazao, mara tulikosa mvua, mara tulikosa nini, nataka niishauri Serikali hebu Ofisi ya TAMISEMI waweke mkakati na waelekezwe Wakurugenzi waje na mawazo mapya ya kukusanya mapato, wasiendelee kutumia vyanzo vya zamani vya kutegemea kilimo peke yake, wajaribu kuwa wabunifu watafute vyanzo vipya vya mapato na Serikali kuu iwasaidie kuwekeza katika miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kwenye uvuvi tuwekeze katika suala zima la uvuvi, kwenye kilimo tuhakikishe mazao yetu yanapata masoko, mazao yetu yananunuliwa , pembejeo zinawahi ili mapato ya nchi yetu yaweze kuimarika na tuachane na tatizo la Serikali za Mitaa kuwa ni tegemezi kwa Serikali Kuu. Najua Wakurugenzi wakipewa maelekezo kwa Madiwani tulionao na wenyeviti wetu wa halmashauli wakithubutu najua inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Mfuko wa Wanawake na Vijana. Naomba nichukue nafasi hii kupongeza Serikali kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Wakurugenzi, Madiwani na Wenyeviti wa Halmashauri kwa kweli wameonesha kabisa tulikadiria kutenga bilioni 60, fedha zilizotolewa ni bilioni 15. Hali siyo nzuri, nazungumza kwa sababu nina uhakika nilikuwa kwenye Kamati ya LAAC kila halmashauri wanaokuja wakuja na maneno matupu, fedha haipelekwi, unaona zimepelekwa bilioni 15 peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukienda kwenye uhalisia, hawaji na vikundi ambavyo vinathibitisha kweli wamepata hizi fedha. Kila siku tukiuliza hapa maswali, Serikali iko kwenye mkakati, tumejipanga, tutahakikisha tunaelekeza, leo nataka nimwone Mheshimiwa Waziri Jafo, atakapokuja kuhitimisha hotuba yake atuambie sheria hii inaletwa lini katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu jambo hili, sio la leo, taarifa ya Mwenyekiti Mheshimiwa Ngombale kwa awamu zote tangu tumeingia kwenye Kamati ya LAAC amekuwa akizungumza na hii taarifa ambayo Mheshimiwa Waziri ametuletea imesema kwamba Serikali ije na sheria, hansard zote nimezitafuta tangu 2010, vitabu vyote hivi leo nimevibeba ninavyo, Kamati ya Bunge ya mzee Zungu na wengine na mpaka ameingia Mheshimiwa Rweikiza na hata jana wameendelea kushauri namna ya kuleta hii sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumechoka na kusikia kwamba tuko kwenye mkakati, kutengeneza mipango, tunataka kusika sasa sheria inaletwa lini hapa Bungeni. Leo nitangaze rasmi kabisa hapa, Mheshimiwa Waziri namheshimu sana, ni mwanangu, nimemlea mwenyewe, nimemtengeneza mwenyewe mpaka hapo alipofika na namjua uwezo wake wa kazi. Nataka nimtangazie rasmi kabisa kwamba kama haji na hii sheria hoja yake sikubaliani nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu Mfuko wa asilimia kumi ya wanawake na vijana ndiyo Mfuko pekee uliowekwa kwa ajili ya kuwakomboa wanawake wanyonge, hawa wanawake walio vijijini hawana fursa ya kufikia mabenki ambayo yana riba kubwa, mashirika mengine hawayawezi kabisa wanawafanyia wao kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Mfuko uliwekwa kwa ajili ya kuwakomboa wanyonge. Nimemsikia amekuja na mkakati wa kuwasamehe riba, lakini tunataka kusikia hii sheria inaletwa lini. Kwa kweli nitawaomba na nitawashawishi Waheshimiwa Wabunge, atakapokuja wakati wa kupitisha vifungu kama haji na majibu kwa kweli mwanangu leo ajiandae kwamba mama yake sasa leo namkwamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niiombe Serikali kuu huu Mfuko wa wanawake na vijana tukitegemea halmashauri peke yake hazitafika popote. Kulikuwa na mfuko ambao Serikali Kuu ilikuwa inatenga, kila mwaka zinapelekwa kwenye halmashauri kuongezea nguvu, lakini miaka mitatu hii mfululizo hakuna kinachotengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunataka leo pia tusikie Serikali ina mkakati gani wa kupeleka hizi fedha kwenye halmashauri kuongezea katika mfuko. Kwa sababu tukitegemea halmashauri zetu na halmashauri zingine ziko hoi kabisa na zingine mapato yake hayatoshi, lakini matumizi yake wakati mwingine yanakuja ya dharura, naomba leo Serikali ituambie huu Mfuko wetu uliokuwepo miaka nenda rudi ukaja ukaondoka katika miaka hii miwili, unarudi lini ili fedha ziende kusaidia wanawake na vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie sekta ya afya na hapa nichukue nafasi hii kwa kweli kumpongeza Mheshimiwa Waziri Jafo na timu yake yote, Waziri mwenyewe na Naibu Waziri, Katibu Mkuu Iyombe na Naibu Katibu Mkuu mama Chaula, naomba nimtaje kabisa kwa jina huyu mama kwa kweli amenishangaza. Sekta ya afya wanafanya kazi vizuri sana katika kitengo hicho, wamepeleka fedha kwa ajili ya kujenga vituo 48 nchi nzima, wamepeleka fedha za kutosha na nimeshavitembelea hivyo vituo, nimeviona, juzi nilikuwa Makete, nikaenda Nyasa nimekwenda kuangalia mwenyewe kushuhudia kama kweli kazi imepelekwa. (Makofi)

Mhshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza sana kwa hii kazi na wananchi wamenituma wanasema ahsanteni sana kwa sababu sekta ya afya ni ukombozi. Hata hivyo, kwa mujibu wa taarifa ya Waziri tunaona kabisa tuna kata zaidi ya 4000 lakini vituo vilivyopo havifiki hapa 600, lakini nimekwenda mbali zaidi nimekwenda kufanya research katika Ofisi ya TAMISEMI wamenipa kitabu hiki chenye mpango mkakati wa mipango yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaona kabisa sekta ya afya ni eneo muhimu sana, vituo vilivyopo havitoshi kuhudumia wananchi. Kwenye Ilani ya CCM tumejielekeza kupeleka kituo cha afya kila kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuomba sana na nimeona mipango ya TAMISEMI wamenipa, hapo wanachohitaji TAMISEMI ni fedha, wanahitaji fedha kwa ajili ya kwenda kujenga vituo vya afya, wanahitaji fedha kwa ajili ya kujenga zahanati, wanahitaji fedha kwa ajili ya kujenga hospitali za Wilaya, lakini wanahitaji fedha kwa ajili ya kumalizia maboma, ambayo yalijengwa na wananchi yako zaidi ya 1800. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nguvu za wananchi zimeishia hapa. Nilimsikia juzi Mheshimiwa Ntimizi anasema yeye amejenga karibu vituo kumi na kitu kwenye kata yake. Nimekwenda juzi Wilaya ya Njombe nimeona. Naomba sasa Serikali na bahati nzuri Ofisi ya TAMISEMI wameshatengeneza mchanganuo kwa kila eneo wanakohitaji fedha wametengeneza wanahitaji fedha katika sekta ya afya kiasi gani, wanahitaji fedha katika hospitali ya Wilaya kiasi gani na katika halmashauri. Tunaomba fedha hizi ziende ili wananchi waweze kupatiwa vituo vya afya na hospitali kwa ajili ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie upande wa Utumishi, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana mzee wetu mzee Mkuchika kwa kazi mzuri wanayoifanya ya kuhakikisha sekta ya uchumi inaleta maendeleo katika Taifa letu. Kwa kweli ni ukweli usiopingika wafanyakazi sasa hivi wanafanya kazi tofauti na zamani, watu walikuwa wakiingia Ofisini kuangalia mitandao, kupiga simu, kwenda kunywa chai, lakini sasa hivi kumekuwepo na nidhamu ya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwapongeza, lakini ni ukweli usiopingika wafanyakazi wa nchi hii na wenyewe wanafanya kazi katika mazingira magumu. Kuna posho zao za kujikimu katika masaa ya ziada ya kazi, manesi wetu wanafanya kazi usiku na mchana Madaktari, wafanyakazi wetu katika Taasisi mbalimbali, Walimu wana madai yao huko, lakini wanafanya kazi kwa weledi, wanafanya kwa moyo na wanafanya kazi kwa uzalendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba katika bajeti inayokuja hii hebu tuwatengee fedha katika kulipa madeni tulipe na madeni ya wafanyakazi wetu ili waendelee kuwa na hali na kuendelea kuiamini Serikali yao na waendelee kuchapa kazi. Kwa kweli hapa naomba tuangalie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la upungufu wa wafanyakzi, sekta ya afya peke yake wafanyakazi kwa upande wa TAMISEMI 66,000, upungufu huo kwenye zahanati kwenye vituo vya afya kila mahali na sijakwenda sekta zingine upungufu wa Walimu hasa wa sayansi na wa hesabu, pia Walimu wa shule za awali hawapo. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa hebu atuambie katika hawa wafanyakazi milioni hamsini mnaosema…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuungana na wenzangu kuweza kuchangia katika hoja hizi mbili Ofisi ya TAMISEMI na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote aliyenipa fursa ya kuweza kusisimama na kuweza kuchangia katika Bunge lako Tukufu. Nitoe pole sana kwa wananchi wenzetu Afrika Kusini kwa kuondokewa na muasisi wetu mama Winnie Mandela. Naomba niungane nao sisi Chama cha Mapinduzi tumepeleka mwakilishi na UWT tumepeleka mwakilishi, tunaomba tuungane nao na Mwenyezi Mungu ampoke na amlaze mahala pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na timu yake yote ya Serikali yake kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya ya kutekeleza Ilani ya CCM kiasi kwamba hata tukifanya uchaguzi hata hizi ndogo zilizopita Chama cha Mapinduzi kinaibuka na ushindi mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni dalili tosha kwamba hata kura zingepigwa leo za Mheshimiwa Rais na hata kura zingepigwa leo za Wheshimiwa Wabunge na hata kura zingepigwa leo za Serikali za Mitaa na hata Madiwani Chama cha Mapinduzi kingepata ushindi wa asilimia 100 kwa sababu wananchi wana imani nacho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumtia moyo Mheshimiwa Rais kuwatia moyo Waheshimiwa Mawaziri wote na hasa TAMISEMI na Utumishi waendelee kuchapa kazi na sisi wanawake wa Tanzania tuko nyuma yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya utangulizi huo, naomba sasa nijielekeze katika mambo machache niliyoyachagua kuyatilia mkazo. Hapa nitaanza na kwa kweli kuipongeza Ofisi ya TAMISEMI chini ya kijana wetu shupavu Mheshimiwa Jafo kwa kazi nzuri sana waliofanya ya kudhibiti matumizi ya fedha na mapato yake. Kwa mujibu wa taarifa ya mkaguzi wa hesabu za Serikali inaonesha kwamba kwa halmashauri zilizokaguliwa 166 halmashauri zimepata hati safi zaidi asilimia 90. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni mkombozi mkubwa sana kwa sababu nilikuwa mjumbe wa Kamati ya LAAC tulikuwa tukiona madudu mengi katika halmashauri, matumizi ya fedha yalikuwa ni ya ovyo, watu walikuwa hawafuati kanuni za fedha, fedha zilikuwa zinaibiwa, lakini kwa usimamizi wa Mheshimiwa Waziri na wenzake kuwa makini naona sasa matokeo mazuri yanakuja. Ni matumaini yangu sasa hata fedha zitakazokaguliwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018 tutapata asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze mpango wa kukusanya mapato ni ukweli usiopingika kiwango kimeongezeka, lakini niseme ukweli bado hakijawa cha kuridhisha. Ni asilimia 50 tu ya mapato yote yaliyokusanywa katika halmashauri, lakini unasikiliza huku Wakurugenzi kilio kingi wanazungumzia sijui mazao, mara tulikosa mvua, mara tulikosa nini, nataka niishauri Serikali hebu Ofisi ya TAMISEMI waweke mkakati na waelekezwe Wakurugenzi waje na mawazo mapya ya kukusanya mapato, wasiendelee kutumia vyanzo vya zamani vya kutegemea kilimo peke yake, wajaribu kuwa wabunifu watafute vyanzo vipya vya mapato na Serikali kuu iwasaidie kuwekeza katika miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kwenye uvuvi tuwekeze katika suala zima la uvuvi, kwenye kilimo tuhakikishe mazao yetu yanapata masoko, mazao yetu yananunuliwa , pembejeo zinawahi ili mapato ya nchi yetu yaweze kuimarika na tuachane na tatizo la Serikali za Mitaa kuwa ni tegemezi kwa Serikali Kuu. Najua Wakurugenzi wakipewa maelekezo kwa Madiwani tulionao na wenyeviti wetu wa halmashauli wakithubutu najua inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Mfuko wa Wanawake na Vijana. Naomba nichukue nafasi hii kupongeza Serikali kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Wakurugenzi, Madiwani na Wenyeviti wa Halmashauri kwa kweli wameonesha kabisa tulikadiria kutenga bilioni 60, fedha zilizotolewa ni bilioni 15. Hali siyo nzuri, nazungumza kwa sababu nina uhakika nilikuwa kwenye Kamati ya LAAC kila halmashauri wanaokuja wakuja na maneno matupu, fedha haipelekwi, unaona zimepelekwa bilioni 15 peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukienda kwenye uhalisia, hawaji na vikundi ambavyo vinathibitisha kweli wamepata hizi fedha. Kila siku tukiuliza hapa maswali, Serikali iko kwenye mkakati, tumejipanga, tutahakikisha tunaelekeza, leo nataka nimwone Mheshimiwa Waziri Jafo, atakapokuja kuhitimisha hotuba yake atuambie sheria hii inaletwa lini katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu jambo hili, sio la leo, taarifa ya Mwenyekiti Mheshimiwa Ngombale kwa awamu zote tangu tumeingia kwenye Kamati ya LAAC amekuwa akizungumza na hii taarifa ambayo Mheshimiwa Waziri ametuletea imesema kwamba Serikali ije na sheria, hansard zote nimezitafuta tangu 2010, vitabu vyote hivi leo nimevibeba ninavyo, Kamati ya Bunge ya mzee Zungu na wengine na mpaka ameingia Mheshimiwa Rweikiza na hata jana wameendelea kushauri namna ya kuleta hii sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumechoka na kusikia kwamba tuko kwenye mkakati, kutengeneza mipango, tunataka kusika sasa sheria inaletwa lini hapa Bungeni. Leo nitangaze rasmi kabisa hapa, Mheshimiwa Waziri namheshimu sana, ni mwanangu, nimemlea mwenyewe, nimemtengeneza mwenyewe mpaka hapo alipofika na namjua uwezo wake wa kazi. Nataka nimtangazie rasmi kabisa kwamba kama haji na hii sheria hoja yake sikubaliani nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu Mfuko wa asilimia kumi ya wanawake na vijana ndiyo Mfuko pekee uliowekwa kwa ajili ya kuwakomboa wanawake wanyonge, hawa wanawake walio vijijini hawana fursa ya kufikia mabenki ambayo yana riba kubwa, mashirika mengine hawayawezi kabisa wanawafanyia wao kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Mfuko uliwekwa kwa ajili ya kuwakomboa wanyonge. Nimemsikia amekuja na mkakati wa kuwasamehe riba, lakini tunataka kusikia hii sheria inaletwa lini. Kwa kweli nitawaomba na nitawashawishi Waheshimiwa Wabunge, atakapokuja wakati wa kupitisha vifungu kama haji na majibu kwa kweli mwanangu leo ajiandae kwamba mama yake sasa leo namkwamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niiombe Serikali kuu huu Mfuko wa wanawake na vijana tukitegemea halmashauri peke yake hazitafika popote. Kulikuwa na mfuko ambao Serikali Kuu ilikuwa inatenga, kila mwaka zinapelekwa kwenye halmashauri kuongezea nguvu, lakini miaka mitatu hii mfululizo hakuna kinachotengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunataka leo pia tusikie Serikali ina mkakati gani wa kupeleka hizi fedha kwenye halmashauri kuongezea katika mfuko. Kwa sababu tukitegemea halmashauri zetu na halmashauri zingine ziko hoi kabisa na zingine mapato yake hayatoshi, lakini matumizi yake wakati mwingine yanakuja ya dharura, naomba leo Serikali ituambie huu Mfuko wetu uliokuwepo miaka nenda rudi ukaja ukaondoka katika miaka hii miwili, unarudi lini ili fedha ziende kusaidia wanawake na vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie sekta ya afya na hapa nichukue nafasi hii kwa kweli kumpongeza Mheshimiwa Waziri Jafo na timu yake yote, Waziri mwenyewe na Naibu Waziri, Katibu Mkuu Iyombe na Naibu Katibu Mkuu mama Chaula, naomba nimtaje kabisa kwa jina huyu mama kwa kweli amenishangaza. Sekta ya afya wanafanya kazi vizuri sana katika kitengo hicho, wamepeleka fedha kwa ajili ya kujenga vituo 48 nchi nzima, wamepeleka fedha za kutosha na nimeshavitembelea hivyo vituo, nimeviona, juzi nilikuwa Makete, nikaenda Nyasa nimekwenda kuangalia mwenyewe kushuhudia kama kweli kazi imepelekwa. (Makofi)

Mhshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza sana kwa hii kazi na wananchi wamenituma wanasema ahsanteni sana kwa sababu sekta ya afya ni ukombozi. Hata hivyo, kwa mujibu wa taarifa ya Waziri tunaona kabisa tuna kata zaidi ya 4000 lakini vituo vilivyopo havifiki hapa 600, lakini nimekwenda mbali zaidi nimekwenda kufanya research katika Ofisi ya TAMISEMI wamenipa kitabu hiki chenye mpango mkakati wa mipango yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaona kabisa sekta ya afya ni eneo muhimu sana, vituo vilivyopo havitoshi kuhudumia wananchi. Kwenye Ilani ya CCM tumejielekeza kupeleka kituo cha afya kila kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuomba sana na nimeona mipango ya TAMISEMI wamenipa, hapo wanachohitaji TAMISEMI ni fedha, wanahitaji fedha kwa ajili ya kwenda kujenga vituo vya afya, wanahitaji fedha kwa ajili ya kujenga zahanati, wanahitaji fedha kwa ajili ya kujenga hospitali za Wilaya, lakini wanahitaji fedha kwa ajili ya kumalizia maboma, ambayo yalijengwa na wananchi yako zaidi ya 1800. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nguvu za wananchi zimeishia hapa. Nilimsikia juzi Mheshimiwa Ntimizi anasema yeye amejenga karibu vituo kumi na kitu kwenye kata yake. Nimekwenda juzi Wilaya ya Njombe nimeona. Naomba sasa Serikali na bahati nzuri Ofisi ya TAMISEMI wameshatengeneza mchanganuo kwa kila eneo wanakohitaji fedha wametengeneza wanahitaji fedha katika sekta ya afya kiasi gani, wanahitaji fedha katika hospitali ya Wilaya kiasi gani na katika halmashauri. Tunaomba fedha hizi ziende ili wananchi waweze kupatiwa vituo vya afya na hospitali kwa ajili ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie upande wa Utumishi, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana mzee wetu mzee Mkuchika kwa kazi mzuri wanayoifanya ya kuhakikisha sekta ya uchumi inaleta maendeleo katika Taifa letu. Kwa kweli ni ukweli usiopingika wafanyakazi sasa hivi wanafanya kazi tofauti na zamani, watu walikuwa wakiingia Ofisini kuangalia mitandao, kupiga simu, kwenda kunywa chai, lakini sasa hivi kumekuwepo na nidhamu ya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwapongeza, lakini ni ukweli usiopingika wafanyakazi wa nchi hii na wenyewe wanafanya kazi katika mazingira magumu. Kuna posho zao za kujikimu katika masaa ya ziada ya kazi, manesi wetu wanafanya kazi usiku na mchana Madaktari, wafanyakazi wetu katika Taasisi mbalimbali, Walimu wana madai yao huko, lakini wanafanya kazi kwa weledi, wanafanya kwa moyo na wanafanya kazi kwa uzalendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba katika bajeti inayokuja hii hebu tuwatengee fedha katika kulipa madeni tulipe na madeni ya wafanyakazi wetu ili waendelee kuwa na hali na kuendelea kuiamini Serikali yao na waendelee kuchapa kazi. Kwa kweli hapa naomba tuangalie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la upungufu wa wafanyakzi, sekta ya afya peke yake wafanyakazi kwa upande wa TAMISEMI 66,000, upungufu huo kwenye zahanati kwenye vituo vya afya kila mahali na sijakwenda sekta zingine upungufu wa Walimu hasa wa sayansi na wa hesabu, pia Walimu wa shule za awali hawapo. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa hebu atuambie katika hawa wafanyakazi milioni hamsini mnaosema…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kipekee nianze kwa kumshukuru Mungu, muweza wa yote aliniwezesha kusimama na kutoa mchango katika hoja hii muhimu ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake yote kwa kuandaa taarifa nzuri na kuiwasilisha vizuri. Kipekee, nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri na timu yake yote; IGP Kamanda Sirro, Kamanda wa Magereza, Kamanda wa Uhamiaji na Kamanda wa Zimamoto kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha nchi ya Tanzania tunaendelea kuishi kwa amani na usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashuhudia kwamba Mamlaka hii ya Mambo ya Ndani wameweza kudhibiti mauaji ya Albino. Ni ukweli usiopingika, wamedhibiti wezi wakiwemo na wezi wa magari; ni ukweli usiofichika, wamedhibiti mpaka na wezi wa mabenki; ni ukweli usiofichika, wamedhibiti mauaji ya raia wasiokuwa na hatia; Albino, vikongwe, Askari wetu waliokuwa mstari wa mbele na hata wananchi wa Kibiti ambao walikuwa wanauawa kama kuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnyonge mnyongeni, haki yake apewe. Hongera sana Kamanda Sirro, hongera sana Makamanda wote. Nataka niwaambie, akutukanaye hakuchagulii tusi; na ukiwa kwenye maji unaoga, akija mwendawazimu usimfukuze, chutama kwenye maji. Atakayewalipa ni Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu, unaona mpaka watu wanatembea, wanaongea na wanazungumza watakavyo ni kwa sababu ya amani. Watu wamekula, wameshiba, wanalala kwa amani mpaka sasa wanavimbiwa wanatukana ovyo. Kamanda Sirro na timu yake wasikate tamaa. Mti mzuri wa maembe ndiyo unaopigwa mawe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wanawake wa Tanzania ambao tumeachwa wajane kule Kibiti, ambao wameachwa wajane kule Rufiji, Albino wasiokuwa na hatia ambao wameachwa wajane au wameachwa yatima, sisi tunawaombea dua kwa Mwenyezi Mungu na ndiye atakayewalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakiona watu wanapiga kelele, wajea wamewashika pabaya. Maana wamedhibiti kila kona. Madawa ya kulevya, waliokuwa wanafanya wengine wako hapa wengine wako nje, wamedhibiti. Mikutano isiyokuwa na tija, watu walikuwa muda wote maandamano, wamedhibiti, hongereni. Ndiyo maana leo unaona sasa kila anayesimama, wanawapiga kwa sababu wamewashika pabaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwatia moyo. Wasivunjike moyo, wasonge mbele, tunatambua kazi yao na Watanzania wanatambua kazi yao na ndiyo maana wanawaombea dua kwa Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika, Jeshi la Polisi limedhibiti ajali za barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea. Jeshi la Polisi limedhibiti ajali za barabarani. Nani ambaye hajui kwamba kwa miaka ya hivi karibuni kulikuwa na ajali za kupitiliza? Kuna watoto wamebaki yatima, kuna wamama wamebaki wajane; kuna familia zimeondoka zote kwa sababu ya mwendokasi. Nani alikuwa hajui?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi wamedhibiti, wameweka mwendo wa taratibu, ajali zimepungua kwa kiwango cha asilimia 35. Nawapongeza, waendelee kuchapa kazi na wakaze buti. Wakiona tunapiga kelele wametushika pabaya, tukiwemo na sisi Wabunge tulikuwa ni miongoni mwa watu tuliokuwa tunakwenda mwendo kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimeshamtangazia dereva wangu, tukikamatwa hiyo kesi ni ya kwako. Endeleeni kudhibiti ili kuokoa Watanzania wanaofariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza kwa sababu wamedhibiti wahamiaji haramu. Nchi yetu ilikuwa inaelekea kubaya kwa sababu Tanzania ni barabara. Nampongeza Kamishna wa Uhamiaji, Mama Anna, kwa kazi nzuri anayoifanya. Wamewadhibiti, wametushika pabaya, kwa sababu baadhi ya wasioitakia mema nchi yetu, walikuwa wanawatumia wahamiaji haramu kuvuruga amani ya nchi yetu. Hongera sana, wapige kazi wala wasiwe na wasiwasi. Sisi tulio wengi tuko nyuma yao na Mwenyezi Mungu atawapa baraka zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara bada ya utangulizi huo, nimemsikia mtoto wangu Lema akieleza hapa. Mimi nimeita mwanangu, analeta propaganda mwanangu. Hivi watu 1,000 wafariki katika nchi hii ya Tanzania; familia za watu 1,000 zipoteze, watu 1,000, tuendelee kuwa hivi mwanangu! Jamani hebu semeni ukweli, msipotoshe umma. Jamani hata kama tunatafuta kick siyo kwa namna hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningetamani Mheshimiwa Lema aje na ushahidi atuoneshe. Kweli familia 1,000 watu wapotee halafu nchi ibaki kuwa hivi? Jamani, hebu waseme ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya utangulizi huo, nijielekeze kwenye michango yangu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, naomba nizungumzie bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani. Tumeona kwamba kuna fedha zimepelekwa zaidi ya asilimia 78. Ninachokiomba ili Taasisi za Mambo ya Ndani ziweze kutekeleza wajibu wao sawasawa, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha kama yuko hapa anisikie. Hebu wapeleke fedha kwenye haya Majeshi waweze kununua vipuli kwa ajili ya magari, waweze kupata fedha kwa ajili ya kununua mafuta, waweze kupata fedha kwa ajili ya kulipa madeni. Taasisi zinafanya kazi kwa hali ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi ni sawasawa na hospitali. Shida haina hodi wala nini. Unapotokea uhalifu, Kamanda wa Mkoa hana mafuta, OCD hana mafuta, Mkuu wa Kituo hana mafuta, wote wanakuwa ombaomba. Naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yake na Serikali iko hapa na Waziri Mkuu yuko hapa. Hebu waipe kipaumbele kinachostahili Wizara ya Mambo ya Ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni Zimamoto. Mfano tu ni Dodoma, wana magari mawili tu, moja liko uwanja wa ndege, moja liko hapa; na hapa ni Makao Makuu. Hivi gari mbili zinatosha kwa Dodoma? Vile vile bajeti ya kwenda kujenga nyumba za Askari hakuna. Naomba hebu Serikali ione Wizara hii ya Mambo ya Ndani ipewe heshima inayostahili ipelekewe fedha kwa ajili ya maendeleo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie nyumba za Askari. Naomba niungane na wenzangu kwa kazi nzuri inayofanywa na Serikali, lakini ni ukweli usiopingika, hali siyo nzuri katika nyumba za Askari wetu. Askari wetu wanaishi katika nyumba mbaya. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kutenga shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kujenga nyumba za Askari; na kwa mujibu wa taarifa, zitajengwa nyumba 400. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, Jeshi la Polisi linalo Kitengo cha Ujenzi, Jeshi la Magereza linalo Kitengo cha Ujenzi; hebu imarisheni vitengo hivi. Sasa hivi vile vitengo vimekufa, matokeo yake sasa tunahitaji kutumia fedha nyingi zaidi tofauti na ilivyokuwa zamani. Na-declare interest kabisa, nami ni mtoto wa Askari na ndiyo maana nikiona mtu anamkejeli Askari huwa naingia na uchungu sana kwa sababu Askari ni mtu aliye mstari wa mbele kupambana usalama wa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokiomba, waimarishe hiki kitengo wakipatie fedha. Bahati nzuri kinao Watendaji wazuri, kinao mainjinia. Kwa sababu sasa hawana kazi, wengine sasa ndio ma- OCD. Mfano OCD wa Ileje, ni injinia yule lakini leo ni OCD; na watu wengine. Hebu waimarishe hiki kitengo kiweze kujenga kwa gharama nafuu ili kwa kutumia na nguvu ya wale wafungwa, tunaweza kuokoa fedha nyingi za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie maslahi ya Askari wetu. Askari wetu wanafanya kazi ngumu sana katika mazingira magumu tena ya hatari. Wanaishi na raia na raia wengine wako humu ndani, wanaona jinsi wanavyozungumza. Hivi akikutana na Askari kwenye kona, itakuwaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Askari hawa tuimarishe ulinzi wao, tuwajengee nyumba za kutosha, tuhakikishe maslahi yao yote wanapata, tuhakikishe wanapokwenda likizo wanapata haki zao, wanapopanda madaraja tunawapa fedha zao. Wapo Askari wamepanda madaraja, hawaongezewi mishahara, mpaka wanastaafu matokeo yake hata pension yao inakuwa ni kidogo. Askari huyu ambaye anatufanyia kazi nzuri, tunamlipa nini? Naomba sana, hebu waangalie kwa macho ya huruma katika jeshi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie suala zima la upandishaji wa vyeo kwa Askari wetu. Nashukuru sana Serikali hii na majeshi yote yameweka utaratibu. Kuna kanuni ya namna ya kuajiri na namna ya kuwapandisha madaraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kabisa, hebu angalieni na wale Askari waliofanya kazi kwa muda mrefu. Wamefanya kwa weledi, kwa uaminifu lakini hawana elimu ya juu. Hawa wanasuasua katika kupanda vyetu, utakuta ni Constable tangu ameanza; akisuasua mara amekuwa Corporal, mara amekuwa Seargent mara amekuwa Major kwa muda mrefu sana. Hivi kwa nini hawa wasipewe heshima kama ambavyo wengine wanavyopata? Kwa sababu wamefanya miaka 25, miaka 30 anabaki kuwa Constable. Hebu naomba hii kanuni iangaliwe tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala zima la posho za chakula cha Askari. Naishukuru Serikali, angalau wamewaongezea Sh.300,000/=. Namshukuru na Mheshimiwa Rais wetu amewapa Sh.100,000/= kwa ajili ya vinywaji. Askari wanashukuru. Nami nazungumza nao, nashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokiomba, hebu Serikali ijaribu kuona uwezekano hata kuwaongezea tena laki moja moja hata zikawa shilingi laki nne, kwa sababu wanafanya kazi nzuri sana, kazi ambayo ni ya kutukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Askari wetu wanaishi uraiani, kwenye nyumba za kupanga; walikuwa wanalipwa posho asilimia 15 kwa ajili ya kulipa kodi ya nyumba, iliondolewa kwa maelezo kwamba wanahakiki. Nataka nijue, huu uhakiki utakwisha lini? Vile vile Askari wa Zimamoto
hawana nyumba kabisa; Askari wa Uhamiaji hawana nyumba kabisa, wa Magereza ndiyo usiseme, wengi wanaishi uraiani. Hivi hawa hii posho yao ya nyumba asilimia 15 ni lini wataipata? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na mafunzo ya Askari. Naipongeza Serikali inafanya kazi nzuri sana ya kuwajengea uwezo Askari wetu. Ombi langu, naomba sasa wajifunze namna ambavyo hasa wale CID wanaoweza kukabiliana na hii mitandao, kwa sababu sasa hivi wizi ulio mwingi ni wa kwenye mitandao. Hawa Askari wetu CID wanajengewaje uwezo ili waweze kukabiliana na changamoto za sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kabisa ambalo nataka nijue, nimepata habari kwamba sasa hivi Askari wanaokwenda kusoma CID, traffic na kozi nyingine wameambiwa sasa wanatakiwa kuchangia kila siku shilingi 7,000/=. Nataka kujua, huo utaratibu umeanza lini? Kwa nini wachangie? Hivi anapoondoka ameiacha familia yake, itakula nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Nishukuru pia Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi na fursa ya kuweza kuchangia katika hoja hii muhimu kwani maji ni uhai, maji ni kilimo, maji ni uchumi, maji kwa kweli ni kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi naomba nianze kwa kuungana na wachangiaji wenzangu kuishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi njema inayoifanya ya kuhakikisha inapeleka maji mijini na vijijini kwa kiwango ambacho kimeripotiwa katika taarifa hii. Ni ukweli usiopingika kwamba kazi ya kupeleka huduma za maji hasa mijini imefanyika vizuri na ndiyo maana hata Mheshimiwa Msigwa mwaka 2010 nilikuwa naye Kamati ya Maji, mara baada ya kuona Serikali ya CCM imepeleka zaidi ya asilimia 99 katika mji wake wa Iringa alifikiria hata ajiondoe kwenye Kamati kwa sababu hali ilikuwa ni nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niungane na mchangiaji aliyemaliza mwanangu Msigwa hebu usiwe na ndimi mbili, ulisema tununue ndege kwa ajili ya uchumi ulipokuwa Maliasili tumenunua, leo unasema tena ndege hazifai. Jana ulisema tujenge standard gauge, leo unasema tena tusijenge, kupanga ni kuchagua. Rais wetu ameamua kupeleka fedha na kujenga miundombinu ya kiuchumi ili kutengeneza fedha sasa za kwenda kujenga miradi ya maji kwa fedha zetu wenyewe bila kutegemea wafadhili. Ni kilio cha muda mrefu cha Wabunge, tulikuwa tunategemea fedha ziletwe na wafadhili, miradi inasimama tunategemea Benki ya Dunia…

T A A R I F A . . .

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nafikiri anataka nisaidie tu kuendelea kutoa elimu kwamba huwezi kudai maji kama huna fedha. Kwa hiyo, miradi inayofanyika hii ya kujenga miundombinu ya kiuchumi lengo lake Tanzania iweze kujitosheleza kwa fedha na kuweza kupeleka maji vijijini, maji mijini na ndiyo maana nimesema kupanga ni kuchagua na nchi yoyote duniani huwezi ukafanya mambo yote kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, jana hapa Mzee Chenge ameeleza vizuri sana kwamba Serikali sasa imeamua kupeleka fedha za ndani kujenga miradi ya maji. Sasa kama huna fedha zako za ndani, hujaimarisha utalii ukanunua ndege, hujajenga miundombinu ya kuleta uchumi, hizi fedha za kupeleka maji vijijini utapata wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka kusema na Wabunge na kwa kweli na Watanzania wanaotusikiliza, mimi ni mama na ni mdau mkubwa wa maji, Ilani ya CCM tumedhamiria kuwatua wanawake ndoo kichwani. Nataka niwahakikishie ni kweli kama ambavyo amesema Waziri kwenye kitabu chake ukurasa wa saba kwamba ifikapo mwaka 2020 tutapeleka miundombinu ya maji kwa kiwango cha asilimia 85. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwahakikishie kwa sababu miradi mingi iko kwenye mchakato na miradi ya maji inajengwa kwa muda mrefu. Kama lipo tatizo la fedha kutumika vibaya, tumpe nafasi Waziri, naungana na Mheshimiwa Bulembo, hatuna haja ya kuunda Tume kwa sababu kuunda Tume unaongeza gharama. Waziri Mheshimiwa Kamwelwe ana nia njema, kwa muda mfupi tumemuona, yuko smart na ni mtu anayefuatilia, waende wakae chini wakokotoe na mimi kwenye mchango wangu wa maandishi nimempa kabisa na njia za kukokotoa kwamba kuna miradi tuliyofadhiliwa na Benki ya Dunia tupate taarifa ni vijiji vingapi, fedha ngapi zilikwenda, vingapi vimekamilika na vingapi bado na hiyo pesa iko wapi na kama ilitumika vibaya waliohusika wako wapi, Waziri anaweza kazi hiyo. Vilevile miradi ambayo inaendelea fedha yake iko wapi, waliomaliza zile certificate walipwe ili ifikapo mwaka 2020 miradi iwe imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kusema kwamba tuendelee kuiamini Serikali yetu ambayo ina nia njema na imejiandaa vizuri. Kama ambavyo Serikali imeweza kupeleka fedha za dawa na fedha za maji tutapeleka kwa sababu ndiyo kipaumbele pia cha Serikali ya CCM. Kama ambavyo tumeweza kujenga shule katika kila kata na siku moja suala la maji litabaki kuwa historia. Kama ambavyo tumeweza kupeleka madawati kila shule na mpaka yamebaki ya ziada tutafanya, kama ambavyo tunafanya miradi mikubwa ya kimkakati ya kuchimba gesi na mingine na mingine. Tuendelee kuwa na imani, imani huzaa imani na subira huvuta heri. Hakuna nchi yoyote duniani inaweza ikaendelea kwa kuwa na miradi mingi na huu ushauri tumekuwa tukiutoa sisi Wabunge kwamba twende na miradi michache inayotekelezeka, lakini ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa niendelee kuishauri Serikali, jamani kilio cha Wabunge wengi mmekisikia na mimi ninayezungumza ni mdau naongea na wanawake. Tunaomba katika mwaka huu wa fedha hii miradi ikamilike na mwaka wa fedha ujao katika vipaumbele mtakavyovipanga maji, maji, maji, maji na bajeti ya maji iwe ni kubwa na fedha zote zipelekwe kama ambavyo zimepitishwa. Nina imani Serikali kwa kuwa ni sikivu wametusikia, kilio cha Wabunge ni kikubwa, kilio cha wanawake ni kikubwa na mimi hivi karibuni nilikuwa vijijini wamesema na mimi nahakikisha tutahakikisha maji yanapelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie mradi wa Mgango - Kiabakari - Butiama. Mheshimiwa Waziri nimefurahi kweli nimeona katika ukurasa wa 37 umezungumziwa. Hivi mnataka Mke wa Baba wa Taifa Mama Maria ndiyo aje kuomba maji hapa? Huu mradi umeanza tangu mwaka 1978, umefanyiwa tathmini miaka 15 iliyopita kupitia wafadhili wa BADEA wametenga USD 32, leo hapa naona mmeandika 30.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi tangu nimekuwa Mbunge huu sasa ni mwaka wa kumi na kitu, tunazungumzia uendelezaji wa huu mradi hivi kuna shida gani na huu mradi? Hivi kweli Mama Maria aje kutuomba maji hapa Bungeni? Nataka nikuombe Mheshimiwa Kamwelwe utakapohitimisha leo uzungumze na wananchi wa Butiama na Mama Maria Nyerere akusikie. Hivi huu mradi wa BADEA unakuja lini? Kama mradi huu haupo, Serikali ina mkakati gani wa kutenga fedha zake za ndani kama ambavyo mmefanya katika miradi mingine, tupeleke maji kutoka Kiabakari - Butiama mpaka Mgango. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jamani Baba wa Taifa alikuwa ni kiongozi, alikuwa hajipendelei, aliangalia Watanzania wote na ndiyo maana mpaka leo hata barabara ya kwenda kwake haijajengwa ndiyo inajengwa sasa, tena mmeweka wakandarasi kumi, tumevumilia tunakubali. Mwalimu aliangalia watu wote, alipeleka maji mpaka Kilimanjaro yanatiririka yenyewe kupitia kwenye milima, hakujiangalia yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali mpo hapa, hizi fedha za BADEA ni lini zinakuja na zipo kwa nani? Nakuomba jioni hii utakapo-windup hapa tuambie ili kama fedha hazipo tukawaambie wananchi wa Butiama, tukaongee na Mama Maria Nyerere kwamba huu mradi wa maji sahau mama hautakuwepo, tuendelee kuchimba maji na kutumia Mto Kialani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona nizungumze hili kwa uchungu kwa sababu nimekaa miaka kumi, huu mradi nimeupigania muda mrefu, Serikali iliniahidi kwamba BADEA ipo na hapa naiona, lakini leo nimesikitika kwamba eti sasa unaenda kufanyiwa tena upembuzi yakinifu, upi na wakati upembuzi yakinifu ulishafanyika. Hebu leo Mheshimiwa Waziri toa kauli yako na sina mashaka na wewe utafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa pia kujua huu mradi utahudumia wananchi wa Kata ya Mgango pale ambapo chanzo kipo, kwa sababu wale wananchi chanzo kinatoka pale lakini hawahudumiwi na mradi huu. Napenda kujua hizi fedha pia zitakazotengwa na BADEA watapeleka maji Kiliba na Tegeluka, Kata hiyo hiyo ya Musoma Vijijini au itaishia hapo peke yake na kupeleka Kiabakari hawa ambao ndiyo wa chanzo cha maji watabaki kuwa watazamaji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujua hii Wilaya ya Musoma Vijiji, Wilaya aliyozaliwa Baba wa Taifa, Wilaya ambayo imeasisiwa miaka mingi iliyopita kutokea Mrangi mpaka Busekela, kutokea Busekela mpaka Kukilango na Bugwema, hivi tatizo la maji ni la nini wakati Wilaya imezaungukwa na ziwa? Nimepekuapekua humu sikuona vizuri, hebu tuambie Wilaya hii ya Musoma Vijijini na Butiama Serikali ina mpango gani kuwafikishia wananchi maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuipongeza Serikali kwa kusikiliza kilio cha muda mrefu cha Wabunge kupeleka huduma ya maji katika Mji wetu wa Musoma na miji mingine mingi hapa nchini, hali sasa hivi ni nzuri ikiwepo na Jiji la Dar es Salaam, napongeza sana. Dar es Salaam sasa miundombinu ya maji imejengwa, hata juzi nilipokuwa kwenye kampeni Kinondoni haikuwa tena hoja, naomba niipongeze Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu sasa naiomba Serikali pelekeni fedha DAWASA na DAWASCO kwa ajlili ya kujenga miundombinu ya maji maana iliyokuwepo imechakaa na mabomba yanapasuka kusababisha upotevu wa maji na kwenye taarifa ya Waziri umesema. Bila kujenga hii miundombinu na pressure ya maji haya yanayokuja kwa sababu ni mengi tutakuwa hatujafanya chochote na maji yatakuwa yanapotea bila sababu yoyote. Ukiwemo na Mji wa Musoma, Bukoba na miji mingine yote ambayo miundombinu yake imechakaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilete ombi maalum huo mradi wa BADEA unachelewa, nawaomba tu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Naunga mkono hoja, ahsante sana. Mengine nimeleta kwa maandishi myazingatie, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote kwa kunipa nafasi ya kusimama na kutoa mchango wangu katika hoja ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na hoja ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora kwa mwaka wa Fedha 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na timu yote ya Serikali kwa kazi nzuri ya utekelezaji wa Ilani ya CCM. Jambo ambalo limesababisha kila unapofanyika uchaguzi mdogo, CCM inapata ushindi wa kishindo, dalili hizi ni nzuri na kama kura zingepigwa leo ushindi wa Rais, Wabunge na Madiwani ungekuwa wa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huu naomba kujielekeza katika hoja nitakazozitilia mkazo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais, TAMISEMI: Mapitio ya utekelezaji wa Bajeti na ukusanyaji wa Mapato na Maduhuli. Upelekaji fedha katika Halmashauri; pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Serikali Kuu kupeleka fedha katika halmashauri zetu kiasi cha trilioni 3.33, sawa na asilimia 50.63 fedha hizi hazikufikia lengo lililokusudiwa. Naiomba Serikali katika mwaka huu wa fedha tuiangalie sekta ya TAMISEMI katika macho mawili hasa katika kupeleka fedha za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapato ya ndani ya halmashauri pamoja na kwamba halmashauri zimekusanya zaidi, ukilinganisha na mwaka jana tofauti Sh.90/= ziliongezeka na makusanyo yote ni asilimia 50 kwa mujibu wa Taarifa ya Waziri, ukurasa wa tisa (9). Bado kazi ya ukusanyaji wa mapato si ya kiwango cha kuridhisha katika baadhi ya halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri katika kukusanya mapato; naishauri Serikali kuzielekeza halmashauri zetu kuendelea na kubuni miradi ya uwekezaji na kubuni vyanzo vya mapato ambavyo havitaleta kero kwa wanawake na wananchi. Hapa pia ningependa Waziri atuambie je, Serikali imejipangaje kuzisaidia halmashauri zetu kufanya uwekezaji mkubwa utakaoleta tija na kuongeza vyanzo vya mapato na kuziondoa halmashauri katika tatizo la kuwa tegemezi kwa Serikali kuu hata kwa kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usimamizi wa fedha za Serikali za Mitaa; kwa mujibu wa Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/ 2017 na Taarifa ya Waziri ukurasa wa 15 inaonesha kati ya Halmashauri 185 zilizokaguliwa, halmashauri 166 sawa na asilimia 90 zimepata hati safi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Waziri na timu yake yote, Wakurugenzi wa Halmashauri zetu na Madiwani kwa kukubali maagizo ya Rais wetu ya usimamizi wa fedha za Serikali. Lengo likiwa kila kinachopatikana kiingie katika Mfuko wa Serikali na
kinatumika kwa kuzingatia taratibu za fedha za Serikali yetu. Hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri tuendelee kuiwezesha Ofisi ya Mkaguzi wa Ndani katika kila Halmashauri ili waweze kutekeleza wajibu wao kikamilifu na kuhakikisha wanapewa ulinzi wa kutosha katika kutekeleza majukumu yao ili wasipoteze ajira zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa pia nipende kujua Serikali imejipangaje kuimarisha vitengo vya ndani vya ukaguzi ili watekeleze jukumu la kufanya ukaguzi wa ndani kwa uhuru na haki bila ya kuingiliwa na mamlaka zao za ajira?

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezeshaji wa wananchi kiuchumi; Mfuko wa asilimia 10 ya Wanawake na Vijana; pamoja na kuzipongeza halmashauri zilitengewa bilioni 15.6 na kutoa mikopo kwa vikundi 8,672 vya wanawake, vijana na walemavu kati ya 18,233.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema wazi kuwa bado lipo tatizo kubwa la baadhi yetu kutotenga, kutoa hata kufuatilia urejeshaji wa mikopo, ushahidi unathibitishwa na Taarifa ya Waziri kuwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018, Mfuko wa Wanawake ulitengewa Shilingi bilioni 61.6 kiasi kilichotolewa ni Shilingi bilioni 15.6 na ilipangwa vikundi 18,233, vikundi vilivyopata ni 8,672.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwa kuwa Mfuko huu wa Wanawake na Vijana katika Halmashauri ndio mfuko pekee ambao ndio mkombozi kwa mwanamke mnyonge asiye na uwezo wa kufikia taasisi nyingine za fedha kutokana na masharti yake, naomba hapa Waziri atupatie majibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi huu Muswada wa Sheria wa kuweka utaratibu wa utekelezaji wa mpango wa kutaja na kutoa asilimia kumi ya wanawake na vijana utaletwa lini hapa Bungeni kwa sababu ni maoni ya Kamati mbalimbali hapa Bungeni. Je, Serikali Kuu ina mpango gani wa kupeleka fedha katika halmashauri kuunga mkono Mfuko huu kwa sababu fedha hazitengwi kikamilifu na hazitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa huduma za afya; kwa mujibu wa Taarifa ya Waziri ukurasa wa 24 – 29 umeonesha kwa ufasaha kuwa hospitali za wilaya zilizopo 120 zinazohitajika 184 sawa na asilimia 65.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vya afya vilivyopo ni vituo 696 sawa na asilimia 15.7 lengo likiwa ni kuwa na vituo vya afya 4,420 na Serikali iendelee na ujenzi na ukarabati wa vituo vya afya 208.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Zahanati; kwa mujibu wa Taarifa ya Waziri, Zahanati zilizopo nchini 6,440 sawa na asilimia 53, lengo ni kuwa na zahanati 12,543.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri ya kuendelea kujenga, kukarabati hospitali za rufaa za mikoa, hospitali za wilaya, vituo vya afya na zahanati. Tatizo la kusogeza huduma ya afya kwa wananchi bado ni changamoto kubwa sana, wanawake bado wanafariki kwa uzazi na watoto chini ya miaka mitano (5) wanafariki dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri; kabla ya kuja hapa Bungeni nilikutana na baadhi ya wanawake na wananchi na hasa wanawake ninaowawakilisha walinituma nije nilete kilio chao cha kuomba kusogezewa huduma za hospitali kama ambavyo Serikali imejenga shule kila kijiji na sekondari kila kata na ili niweze kuwasilisha maombi yao Bungeni nikianza na TAMISEMI kutaka kujua mipango yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya TAMISEMI chini ya Mtendaji wake mahiri Mzee Iyombe na Chaula walinieleza mipango yao ambayo ni mizuri sana, wanachohitaji Ofisi ya TAMISEMI ni kupatiwa fedha. Ofisi ya TAMISEMI wameishaandaa bajeti ya ujenzi wa zahanati 2,277, vituo vya afya 156 na ukamilishaji wa maboma yaliyojengwa na wananchi 1845 kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukarabati wa vituo vya afya 156 na ununuzi wa vifaa tiba 156 x 850,000,000 = 132,600,000,000/=. Ukarabati wa zahanati angalau nusu ya mahitaji 2,277 x 100,000,000 = 227,700,000,000/=. Ukamilishwaji wa maboma 1,845 = 934,000,000,000/= hivyo Jumla kuu 1,294,300,000,000/=.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri; naiomba Serikali ya CCM itafute fedha hizo Sh.1,294,300,000,000 na kuzikabidhi TAMISEMI kwa ajili ya ujenzi wa miradi hii na kuboresha huduma za afya, kupunguza vifo vya watoto na wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Sekta ya Elimu. Usimamizi wa elimu ya msingi na sekondari nchini; naishukuru Serikali kwa mpango wa kuendelea kuboresha elimu hapa nchini pamoja na pongezi nashauri yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iweke mpango mzuri wa kuwaandaa Walimu wa shule ya awali kwa baadhi ya shule wanaofundisha shule za awali hawana taaluma ya elimu ya awali. Serikali iandae vitabu vya kufundisha na kujifunza kwa wanafunzi wa shule ya awali. Shule za sekondari na msingi zina upungufu wa Walimu na hasa Walimu wa sayansi. Serikali kwa kushirikiana na wananchi wajenge madarasa yatakayopunguza msongamano wa watoto wetu katika shule zetu. Serikali kwa kushirikiana na wananchi itafute fedha kwa ajili ya matundu ya vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iimarishe Kitengo cha Ukaguzi ili kitekeleze wajibu wake kikamilifu. Serikali iendelee kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za Walimu. Ningependa kujua pia mpango wa Serikali wa kukabiliana na changamoto nilizozitaja hapo juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sekta ya Utumishi; pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya kuajiri watumishi katika kada mbalimbali upo upungufu wa watumishi katika kada mbalimbali za umma mfano; Walimu wa shule za awali, Walimu wa shule za msingi na sekondari hasa Walimu wa Sayansi na Hesabu. Maafisa Ugani, Maafisa Maendeleo ya Jamii, Sekta ya Afya, Madaktari, wataalam mbalimbali, Sekta ya Afya TAMISEMI, upungufu ni wafanyakazi 62,976 sawa na asilimia 55. Hapa ningependa kujua hawa wafanyakazi watakaoajiriwa mwaka huu wa fedha 2017/2018 ni wa kada gani na ni wangapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF); napenda kuchukua nafasi hii kuupongeza Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF kwa kazi nzuri ya kutoa huduma za jamii na kuzitambua kaya maskini 1,363,448 tangu kuanza kwa mpango huu na kaya 1,118,751 zenye watu watano na shilingi bilioni 185 zilizotolewa kwa kaya maskini Tanzania Bara na Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi nashauri, Serikali ifuatilie kwa karibu viongozi wanasiasa katika vitongoji, vijiji na kata kwani yapo malalamiko ya baadhi ya wananchi kuwa baadhi ya viongozi wanasiasa wanatambua watu wahitaji kwa upendeleo bila kuzingatia vigezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyombo vya usalama na TAKUKURU: Usalama; nawapongeza kwa kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa salama na amani endelevu na kazi ya kuhakikisha usalama wa viongozi, wananchi na Taifa letu la Tanzania linaendelea kuwa salama na amani na kuwa mfano wa kuigwa katika mataifa mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi, nashauri vyombo vyote vya ulinzi na usalama viendelee kuimarisha ulinzi na usalama na katika nchi yetu na Tanzania iendelee kuwa kisiwa cha amani na utulivu, kwani amani itakapotoweka watakaoumia ni wanawake na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAKUKURU; nawapongeza kwa kazi nzuri wanayofanya ya kudhibiti vitendo vya rushwa na kuwezesha kuokoa fedha nyingi ambazo zilipotea. Ushauri wangu waendelee na kazi ya kupambana na rushwa kwa nguvu na bidii zaidi kwa manufaa ya Taifa letu. Sisi wanawake wa Tanzania tunawaunga mkono katika jitihada hizo za kupambana na rushwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia maeneo machache…

SPIKA: Dakika 10.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, dakika 10? Ahsante sana kwa huo muda kwa sababu nilikuwa najaribu kuangalia dakika tano hizi.

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kutoa mchango wangu katika sekta hizi tatu. Kwanza kabisa kabisa naomba nianze kuungana na Watanzania wenzangu kutoa pole sana kwa akinamama, akinababa na jamii ya Wananjombe kwa misiba mikubwa iliyotokea ya mauaji ya watoto wetu wasiokuwa na hatia. Natoa pole kwa sababu msiba huu ni mkubwa, ni msiba wa Kitaifa na hapa naomba nitoe ushauri kwamba, Serikali yetu ifanye kila jitihada inayowezekana ili wale waliohusika na mauaji yale waweze kupatikana.

Mheshimiwa Spika, mwaka fulani yalitokea mauaji ya wanawake Mkoa wa Mara, Serikali ilichukua hatua na mauaji yalikomeshwa. Mwaka fulani yalitokea mauaji ya maalbino, Serikali ilichukua hatua na mauaji yalikomeshwa. Hivi karibuni tuliona Rufiji mauaji yalikomeshwa na hivi karibuni tuliona watu wenye ulemavu wakifanyiwa ukatili, walikomeshwa, naomba na kule Njombe Serikali ichukue hatua za haraka, ili mambo haya yaishe.

Mheshimiwa Spika, naomba niungane na Wajumbe wenzangu wa Kamati hizi mbili, Kamati ya UKIMWI na Kamati ya Huduma za Jamii, lakini pia niungane na wengine wote waliounga mkono hoja. Hapa nami naunga mkono hoja na kwa kuokoa muda naomba niishauri Serikali kwamba, Maoni ya Kamati ya Masuala ya UKIMWI, kama ambavyo tumeleta mapendekezo, yapokelewe na yafanyiwe kazi.

Mheshimiwa Spika, tumezungumzia tozo ya kupata fedha kwa ajili ya kununua dawa za watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI kwa ajili ya kufubaza. Tusiendelee kutegemea wafadhili kupitia fedha na maeneo mengine kwa sababu, kuna siku hawa wafadhili watasitisha na litakuwa ni janga kwa Taifa letu. Kwa sababu, tulishaanzisha Mfuko ni vizuri sasa Mfuko huu ukaboreshwa na Serikali ikaandaa utaratibu wa kuleta sheria na tukawa na tozo maalum.

Mheshimiwa Spika, pia, tumependekeza kwenye Kamati yetu ya UKIMWI kwamba, umri wa mtoto anayeweza kwenda kupima kwa hiyari bila kwenda na mzazi ufanyiwe marekebisho kulingana na wakati tulionao wa sasa. Badala ya kuwa miaka 18 mpaka kuendelea ianzie miaka 15 waweze kupima kwa sababu, taarifa ambazo Wizara imetuletea kupitia Kamati ya UKIMWI hali ni mbaya, watoto wetu kuanzia miaka 10 mpaka 15 mpaka 25 kila wananchi wanaopimwa asilimia 40 ni watoto wadogo. Kwa hiyo, naungana kabisa na Kamati kwamba, sasa Muswada uletwe hapa Bungeni tufanye marekebisho, sheria tuitunge ili sasa hata hawa watoto wadogo waweze kwenda kupima kwa hiyari kwa ajili ya kuwanusuru.

Mheshimiwa Spika, tumeleta mapendekezo, tunaishauri Serikali ilete sheria ya kuhakikisha suala la bima kwa wote linatungiwa sheria. Tumekwenda Rwanda, Kamati baadhi ya wajumbe walikwenda, wametuletea mrejesho; wenzetu katika suala la bima wako vizuri na sisi Tanzania tuige mfano wake, kuna wengine wamekwenda Ghana wametuletea mfano. Nami naomba nitoe mapendekezo hapa na niungane na Kamati kwamba, sheria ije sasa, ili wananchi wote wapate bima kwa ajili ya manufaa yetu na wewe mwenyewe juzi ulikuwa ukisisitiza, naomba niunge mkono hapo iletwe kwa ajili yetu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie sasa suala zima la ujenzi wa hospitali za rufaa, hospitali za mikoa, hospitali za wilaya na hata vituo vya afya. Hapa naomba nilete pongezi na shukrani nyingi sana kutoka kwa wananchi wa Mkoa wa Mara. Mkoa wa Mara tulikuwa tunajenga hospitali ya kwanza ya Mwalimu Nyerere Memorial Centre, hospitali hiyo ilijengwa kwa muda mrefu na ilikuwa haikamiliki, lakini kwa uongozi wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, sasa hivi hospitali inakwenda mbio na Serikali inatuletea fedha.

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru sana Waziri Mheshimiwa Ummy ameshatembea, ameshaona jitihada zinazoendelea na ameshapewa gharama na ili jengo liweze kuanza zinahitajika kiasi gani. Naomba nitoe ombi tena kwa niaba ya wananchi wa Mara, hebu Mheshimiwa Ummy au Serikali ituletee hizi fedha ili jengo liweze kukamilika hasa hili la mama na mtoto ili kituo kile cha Mwalimu Nyerere Memorial Centre kiweze kufanya kazi na kuwahudumia Wananchi wa mkoa wa Mara.

Mheshimiwa Spika, tunaleta pongezi zetu kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi tumepata fedha bilioni 1.0 kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Rorya; bilioni 1.5 kwa ajili ya kujenga Musoma Vijijini; bilioni 1.5 kwa ajili ya kujenga Tarime na maeneo mengine; lakini tumepata 400 kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Serengeti; na 400 kwa ajili ya kujenga hospitali Butiama. Ombi langu, hii Hospitali ya Butiama na hapa naomba wanisikilize vizuri, najua Mheshimiwa Waziri atakapokuwa aki-wind up atachangia; Hospitali ya Butiama naomba tuipe upekee wa utofauti kabisa. Hospitali ya Butiama ni hospitali ya kihistoria, ni hospitali ambayo Baba wa Taifa alikuwa anatibiwa hapo, ni hospitali ambayo Mama Maria Nyerere akiwa Kijijini Butiama akiugua ghafla ndiko anakotibiwa na ni hospitali ambayo kwa wilaya nzima ya Butiama ndio wilaya inayohudumua wananchi wote zaidi ya watu 200,000.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Butiama ina kituo kimoja tu cha afya kwa sababu, Mwalimu Nyerere alipokuwa Rais aliangalia Watanzania wote, aliwahudumia bila ubaguzi, hakujiangalia nyumbani kwake. Naomba katika misingi ya kumuenzi Baba wa Taifa hebu tuiboreshe Hospitali ya Butiama kwa sababu hata wageni wanaokuja kutembelea Kaburi la Baba wa Taifa wanaougua wanakwenda pale, lakini hata familia ya Baba wa Taifa yenyewe akina Makongoro na wenzake na hata Madaraka anayetulindia Makumbusho ya Baba wa Taifa akiumwa anatibiwa pale Hospitali ile ya Butiama haina hadhi ya kuendana na kazi aliyoifanya Baba wa Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Serengeti wamechangishana fedha wamefika zaidi ya milioni 300 wakaanza kujenga hospitali, kama sio ya kwanza Kitaifa inaweza ikawa ya pili kwa mfano, ni hospitali kubwa na ni nzuri wananchi wamejitolea. Tunashukuru Serikali imetuletea shilingi milioni 400, naomba na hii hospitali hebu waiongezee na yenyewe ifike bilioni 1.5 kama ambavyo wamefanya kwingine.

Mheshimiwa Spika, nimesema mimi hapa leo ni shukrani maana maoni mengi kwenye Kamati yametolewa. Naomba nilete shukrani za wananchi wa Mkoa wa Mara, wametujengea na kuviboresha vituo vya afya 10, shilingi zaidi ya bilioni 6.0, tumepata katika mkoa wetu. Naleta shukrani za wananchi wa Mkoa wa Mara na hata kura zikipigwa leo Chama cha Mapinduzi na Rais wetu watapata ushindi wa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, ombi letu na hapa nataka niongelee kwa Tanzania nzima ikiwemo Kongwa, Mbeya na maeneo mengine; suala la wafanyakazi au watumishi katika hivi vituo vya afya ambavyo vimeboreshwa; naomba Serikali tupeleke watumishi, kama hatukupeleka watumishi ni sawasawa na kufanya kazi bure. Hivi karibuni nimetembelea vituo vyote ambavyo vimepelekewa fedha, nimeenda kuona mafanikio na kusikiliza changamoto, nimejionea mwenyewe Kituo cha Nata nakitolea mfano, Daktari yuko mmoja peke yake wakati chumba cha theatre wanatakiwa wawepo Madaktari wanne; yeye ndio anashika mkasi, yeye ndiye anaandaa gloves, yeye ndiye anafanya kila kitu, yeye ndiye apige kaputi, Daktari mmoja!

Mheshimiwa Spika, aliniletea kilio akasema mama mnatuua, tumeboresha hospitali, tumejenga theatre, tumeweka vifaa tena vya kisasa, vingine tumekuta vimesimama havifanyi kazi kwa sababu, hata wa kuviwasha na kuendesha hiyo mitambo hawapo. Nimekuta baadhi ya mashine hata kujua pass word ikoje mtaalam anasema hajui. Kwa hiyo, nashauri kama alivyosema Waziri wa Utumishi asubuhi kwamba, kipaumbele ni kupeleka watumishi katika zahanati mpya na katika vituo vya afya. Hapa nashauri hivi vituo vya afya 350 walivyoviboresha Serikali yetu ya CCM, naomba na vyenyewe vipewe umuhimu wa kwanza kwa sababu, bila ya kufanya hivyo itakuwa ni sawasawa na kazi bure, wagonjwa watakwenda pale hakuna huduma, hakuna wataalam na kazi ambayo tumeifanya itaishia kwa kweli, kuwa sio nzuri.

Mheshimiwa Spika, naomba niongezee kwamba, kama ambavyo amesema mchangiaji Mheshimiwa Maige na Mkoa wa Mara pia ni miongoni mwa watu ambao wanafanya kazi sana. Sisi Mkoa wa Mara tunajenga majengo ya Serikali na huduma za jamii kwa kitu kinaitwa lisagha, yaani watu wa rika, umri wa kwangu tunapewa boma letu, umri wa mwingine wanapewa boma lao tunajenga kuanzia msingi mpaka lenta bila kutegemea msaada wa Serikali. Tumejenga maboma ya zahanati zaidi ya 100, tumejenga vituo vya afya zaidi ya 100, tumejenga sekondari zaidi ya 100… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, tunaomba hivi Serikali ikijaribu kutenga fedha kukamilisha haya majengo, ili kuunga mkono nguvu za wananchi ambao sasahivi wameishiwa, naleta ombi maalum; kengele ya kwanza hiyo…

SPIKA: Tayari muda wako umekwisha.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Hivi tayari?

WABUNGE FULANI: Ndiyo.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana na naomba kuwasilisha. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu, na kwa kuwa muda ni mfupi, naomba moja kwa moja niende kuunga mkono mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sababu za kuunga mkono hoja ni kwamba Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na watendaji wake chini ya Waziri, Mheshimiwa Engineer Gerson Lwenge, watendaji wote wa Mamlaka za Maji nchini wanafanya kazi ya kupigiwa mfano. Ni ukweli usiopingika kwamba Waziri na timu yake wako vizuri na wanafanya kazi nzuri, fedha zote wanazozipata wanakwenda kutekeleza miradi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, zipo changamoto mbalimbali ambazo Serikali inatakiwa izifanyie kazi na ninaomba niungane na Wabunge waliozungumza kwamba upo sasa umuhimu wa kuhakikisha fedha zote zinazotengwa na Serikali zinapelekwa kama zilivyopitishwa. Kwa sababu huwezi kumlaumu Waziri, huwezi kulaumu watendaji kama hujawapelekea fedha za kutosha. Tunatenga fedha hapa, lakini fedha haziendi kama zinavyokusudiwa na taarifa inaonesha imepelekwa kwa asilimia 19.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishukuru sana Serikali kwa kuimarisha miundombinu ya maji katika Jiji la Dar es Salaam na Pwani, lakini vilevile na Mkoa wa Mara.

Ushauri wangu, naomba niishauri Serikali, ule mradi wa maji Pwani – Dar es Salaam pia uhudumie wananchi wa Mkuranga na Kisarawe kwa sababu pia miundombinu inatoka kule. Vilevile niwapongeze kabisa kwa dhati Mamlaka ya DAWASA kwa kazi nzuri sana ya kusimamia miundombinu ya maji maana kama wasingejenga inawezekana pesa zingepotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee niwapongeze DAWASCO kwa kazi nzuri ya uendeshaji, na ushauri umetolewa kwamba ipo haja ya kuangalia mamlaka hizi na kuziunganisha na mimi naungana nao. Pamoja na hayo naomba nitoe angalizo kwa Serikali, tusikurupuke. Kwa sababu mimi ninayezungumza nilikuwa Mjumbe wa Bodi ya DAWASA miaka tisa na nyuma huko tulikuwa na NUWA na baadaye tukaja na City Water na baadaye tumekuja na DAWASCO, tuliona Mamlaka ya DAWASA ibaki ijenge miundombinu, itafute fedha isimamie miradi na DAWASCO wabaki kuwa waendeshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ushauri wangu, naomba kabla ya kufikia kuziunganisha hizi mamlaka hebu angalieni historia ilikuwaje mpaka zikawa sasa mamlaka mbili kwa lengo la kubana matumizi. Hoja ni nzuri, lakini tusikurupuke, tuifanyie kazi polepole ili tulete tija tusije tukarudi kule nyuma ambapo tulikuwa tumetoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishukuru sana Serikali kwa kuimarisha miundombinu katika Mji wa Musoma, naomba niishukuru sana maana sasa Musoma tunakwenda kupata maji ya kutosha. Ushauri wangu pale chanzo cha maji kinapotoka Mji wa Musoma kinatoka pia Musoma Vijijini. Ninaomba kata ya Etaro, kata ya Nyegina, kata ya Nyakatende na wenyewe wapate maji kutokana na chanzo kile. Tukiacha bila kupata maji wale wananchi wa lile eneo wanaweza wakaharibu ile miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niongelee Mradi wa Bitiama – Kyabakari – Mgango, mradi wa kihistoria, mradi wa kwa Baba wa Taifa, sasa ni miaka 30 mimi nausikia mradi huu. Ni juzi hapa niliusikia wakati Mwandosya akiwa Waziri, amekuja Mheshimiwa Dokta Mwakyembe ameuzungumza, leo anauzungumza Mheshimiwa Engineer Lwenge.

Mheshimiwa wenyekiti, nimepitia kwenye kitabu hiki upembuzi yakinifu umemalizika taarifa imepelekwa BADEA, na mwaka uliopita ilikuwa ni hivyohivyo. Nataka leo Serikali ituambie, hivi kama leo BADEA hawatoi fedha Serikali ina mkakati gani na hasa kwa kuzingatia kule maji yanakwenda mpaka kwa Baba wa Taifa, Baba wa nchi hii ambaye ametufanya wote tuko kama hivi tulivyo? Wananchi wa kule wana adha kubwa sana, wamezungukwa na mito, wamezungukwa na maji, lakini hakuna kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane na wenzangu wote waliosema tozo ya maji iongezeke, na mimi naungana nao kwa sababu tumeona kile kiwango cha shilingi 50 kwa kila lita ya mafuta imeleta tija sana kwa nchi yetu. Naomba iongezeke shilingi 100 ili wanawake wa Tanzania wapunguziwe adha wanayoipata, wanawake wanatembea umbali mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefanya utafiti nimegundua hata wanawake wanaojifungua kabla ya kufikisha umri tatizo ni maji, hata wanawake wanaozaa watoto bila kufikisha umri tatizo ni maji, mimba zinazotoka mpaka watoto wanafariki ni maji kwa sababu wanatembea muda mrefu kwenda kutafuta maji wakati wataalam wanawashauri wapumzike. Vifo vya watoto wanaofariki chini ya miaka mitano asilimia 40 ni watoto wanaozaliwa kabla ya umri na tatizo kubwa ni kwa sababu wanawake wanafanya kazi za shurba. Ataenda kutafuta maji, arudi akalime, arudi akamuhudumie baba, arudi akapike. Jamani, sheria inasema ni umbali wa mita 400 tu, ninaiomba Serikali isiwe na kigugumizi katika kuongeza tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena tumefanya research kabisa sisi wenzenu tumekwenda, wananchi hawana shida kuongezewa shilingi 100, tena haitaleta madhara yoyote katika kuongezeka mfumuko wa bei na kuongezea wananchi mzigo wa maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu aliye na gari ni kidogo ana maisha mazuri na wananchi wakiona matokeo wako tayari kuchangia shilingi 100. Ninaomba tusiogope, hebu twende na mpango huu, ije Finance Bill hapa Bungeni tuipitishe kwa kauli moja twende kuwakomboa wanawake na wananchi… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana, Mungu akubariki sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli nilitaka kusema kama ni dakika tano niongee kesho kwa sababu nina salamu za wanawake wa Tanzania ambao mimi ndiyo wapiga kura wangu.

MWENYEKITI: Basi utaongea kesho, Mheshimiwa Mbogo malizia dakika kumi hizo. Mheshimiwa Richard Mbogo, umejitoa? Sikusikii, naona unainama, unakaa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ameomba niendelee, amenipa zake zimekuwa kumi.

MWENYEKITI: Haya.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na nimshukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Mbogo na nichukue nafasi hii kukupa pole na msiba mkubwa uliokupata wa kuondokea na mama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaona maneno mengi yanazungumzwa humu ndani sasa nimesimama Mbunge ninayewakilisha wanawake wa Tanzania na Jimbo langu ni Tanzania nzima. Hapa naleta salama za wanawake wa wa Tanzania ambao wamekuwa wakifariki kwa kujifungua kwa sababu ya kukosa huduma, ambao wamekuwa wakitembea umbali mrefu kwenda kutafuta huduma za afya, ambao vituo vilikuwa ni duni havitoi huduma kikamilifu, wakienda leba wanafariki, kwa uongozi wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli Serikali imewajengea vituo zaidi ya 350.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamenituma nilete salama za ahsante kwa Mheshimiwa Rais. Wanasema ahsante kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi na wanamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na wanasema achutame maana ukiwa kwenye maji unaoga akija mwendawazimu haumfukuzi na akutukanaye hakuchagulii tusi. Wanaosema Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli hajafanya kitu tuwasamehe maana hawajui watendalo, ndiyo salamu walizonipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanamshukuru Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu Mikoa ya Geita, Simiyu, Kigoma, Mwanza, iko sita ambayo wanawake walikuwa wanafariki kwa kujifungua kwa sababu ya kukosa huduma, kwenye taarifa ya Mheshimiwa Jafo imeeleza ambavyo Serikali inakabiliana na changamoto hizo. Kwa hiyo, ukisikia mtu anabeza tena bahati mbaya wanaongea ni wale ambao hawakwenda leba, tunasema akutukanaye hakuchagulii tusi na ukiwa kwenye maji unaoga akija mwendawazimu haumfukuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumwambia Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli endelea na kazi, tunakuona unahangaika Nyanda za Juu Kusini, leo umefungua vituo vya afya, umekwenda Mikoa ya Mtwara, leo uko Njombe, umekwenda Ruvuma na unakwenda Katavi, unakwenda Tanzania nzima kuwaletea wananchi maendeleo. Chapa kazi baba, tuko nawe na wanawake wa Tanzania na leo nimekuja na book hili ndiyo kazi ulizozifanya na nimewauliza wanasema tukipiga kura leo anashinda kwa asilimia 100. (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema atapita bila kupingwa.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, napenda kuchukua nafasi hii…

MWENYEKITI: Kuhusu Utaratibu.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti...

MWENYEKITI: Kanuni.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni ya 64(1)(a), inasema: “Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 100 ya Katiba yanayolinda na kuhifadhi uhuru wa mawazo na majadiliano katika Bunge, Mbunge, hatatoa ndani ya Bunge taarifa ambazo hazina ukweli”. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa anayechangia ametoa taarifa ambazo si za kweli. Tunajua kwamba Tanzania tuna kata zaidi ya 4,000 na kwa Sera ya Afya inatakiwa kila kata iwe na kituo cha afya. Kwa takwimu tu alizozitoa mwenyewe amesema vimejengwa vituo mia tatu thelathini na kitu na nadhani vilikuwa kama 400 hivi. Kwa hiyo, ukitoa utaona zaidi ya kata 3,000 ambazo zina suffer wanawake wanakufa. Hata ukipitia taarifa vifo vya mama na mtoto ni vingi sana kama Taifa bado hatujavipunguza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na kwamba amepotosha anazungumzia wanawake wote ambao…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Mheshimiwa kaa chini.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Mheshimiwa kaa chini. Mheshimiwa Makilagi, endelea. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, inabidi nicheke tu kwa sababu ni mwanangu ana stress naomba tumsamehe kwa sababu ni juzi tu alikuwa na shida. Mimi kama mama nina kazi ya kufanya counseling nitaendelea kwa sababu kama angekuwa…..

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ana uchungu na anajua kuna pengo angeanza kuonesha Tarime ambayo inapata fedha nyingi kutokana na madini lakini…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, afute kauli yake.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee nimesema kama mama nitaendelea kumlea mwanangu, nitazungumza naye…

MBUNGE FULANI: Afute kauli yake.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Ni juzi alikuwa na shida nahitaji kumsaidia.

WABUNGE FULANI: Afute kauli yake.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kwa kusema kwamba Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amefanya kazi nzuri…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mheshimiwa Salome Makamba last warning.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Kiti hakijasikia bado.

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Maryam, kaa chini.

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikae vipi chini?

MWENYEKITI: Hutaki kukaa chini?

MBUNGE FULANI: Huyo mama ajiheshimu.

MWENYEKITI: Sema tena hutaki kukaa chini?

WABUNGE FULANI: Sema.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Makilagi, endelea na mchango wako.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba niendelee kujielekeza katika mchango wangu kama ambavyo nimejiandaa. Naendelea kumpongeza Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi mzuri, Tanzania nzima maana kwenye Ilani ya CCM aliahidi na ametekeleza kwamba tutajenga sekondari, shule za msingi, watoto watasoma bure na ukisikia watu wazima wanapiga kelele wameshikwa pabaya, leo nimekuja na takwimu zinazoonesha kila shule imepata nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Mkoa wetu wa Mara peke yake Serikali yetu imetupelekea zaidi ya shilingi bilioni 1.7; kwenye hospitali zetu zote za Wilaya kila kila Halmashauri tumepata shilingi bilioni 1.5; kwenye vituo vya afya, hivi ninavyozungumza anajiandaa kujenga siyo hivi vilivyomalizika sasa hivi vingine vipya kwenye Mkoa wa Mara peke yake shilingi bilioni 2 zinakwenda na Mikoa yote ya Tanzania karibu shilingi bilioni 65. Tumpe nini Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli zaidi ya kumpa kura za ndiyo uchaguzi utakapofika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi na nichukue nafasi hii kuipongeza Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya maelekezo ya Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli alisema tuwawezeshe wanawake kiuchumi. Tumewahamasisha wamejiunga katika vikundi vya vijana na wanawake na watu wenye ulemavu na kupitia Bunge hili tulipitisha sheria ili sasa suala la kutoa fedha kwa asilimia kumi ya wanawake na vijana isiwe jambo la hiari liwe ni la lazima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kusema karibu Halmashauri nyingi zinafanya vizuri. Hata hivyo, naomba nitoe ushauri, kuna Halmashauri wanakaidi kutekeleza agizo hili, naomba nitumie nafasi na Mheshimiwa Jafo tunakuamini ni mtendaji hodari na mahiri, hebu orodhesha Halmashauri zote ambazo zimeshindwa kutekeleza Azimio la Bunge na matakwa ya sheria ya kutenga asilimia 10 kwa ajili ya vikundi vya wanawake na vijana ili hatua zinazostahili ziweze kuchukuliwa na vikundi vya wananwake na vijana viweze kupata mkopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Halmashauri zetu ziko taabani, hazina vyanzo vizuri vya mapato kutokana na hali halisi ya Mikoa yao. Nashauri…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Makilagi kwa mchango mzuri. (Makofi)

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, mengine nitachangia kwa maandishi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nimshukuru Mwenyenzi Mungu muweza wa yote aliyenipa fursa ya kuweza kusimama kutoa mchango katika Wizara hii nyeti, Wizara ambayo kwangu mimi naiita moyo wa taifa kwa sababu bila amani hakuna chochote tunachoweza kufanya katika taifa letu. Naomba nipingane na wale wote wanaosema majeshi yetu ikiwepo Jeshi la Polisi kwamba ni ugonjwa wa kansa, mimi naendelea kusema Mwenyezi Mungu awasamehe kwa sababu hawajui watendalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na naomba nipingane na wale wote wanaosema majeshi yetu ikiwemo Jeshi la Polisi kwamba ni ugonjwa wa kansa, naendelea kusema Mwenyezi Mungu awasamehe kwa sababu hawajui watendalo. Na wote hawa wanaozungumza ni kwa sababu hawajawahi kuchimba handaki, hawajawahi kulala kwenye handaki, hawajahi kushuhudia vita ndio maana leo wakisikia mtu amekamatwa wanasema amani hakuna lakini kumbe kuna watu ambao hawalali kwa ajili yetu na si wengine Jeshi la Polisi ni Jeshi la magereza, jeshi la uhamiaji ni jeshi la zima moto. Ninawaomba muwasamehe maana hawajui watendalo na akutanaye hakuchagulii tusi na ukiwa kwenye maji unaoga akija mwendawazimu haumfukuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri Kangi Lugola na timu yake yote kwa kazi njema wanayoifanya. Kusema ukweli mnyonge mnyongeni haki yake apewe, Mheshimiwa Kangi na timu yako na taasisi zako zote mnafanya kazi nzuri na ndio maana leo Wabunge tunazungumza tutakavyo kwa sababu amani imedumishwa mnalinda mali na raia, mnazima moto tunapopata majanga, mnatulinda na katika mipaka yetu ndio maana leo tunasema Mungu awape Baraka zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Kangi kwa kuandaa ripoti nzuri na timu yake kwa kweli taarifa hii ya Wizara ya Mambo ya Ndani imeandaliwa vizuri, imechanganuliwa vizuri ninapongeza kweli inajieleza yenyewe na sio tu na kazi inafanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi pia naishukuru Serikali kwamba kwa bajeti iliyokwisha 2018/2019 ilipeleka fedha vizuri kwenye Wizara ya Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani kwa kiwango cha asilimia 86 nimejaribu kupiga heshabu hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka nitoe ushauri. Wizara hii ya Mambo ya Ndani ndio moyo wa Taifa letu, ninaomba Serikali mko hapa mnisikie tutenge fedha za kutosha kwa ajili ya wizara hii. Wizara hii ina majukumu makubwa sana ya dharura ambayo hata hayatarajiwi, unamkuta OCD yuko Kiteto anaongoza kilometa zaidi ya 200 lakini mafuta anayopewa kwenye gari ni lita 100 kwa mwezi. Lakini unakuta hata service za magari wanatakiwa kwenda doria watulinde Wabunge, walinde doria, watembee kwenye mipaka yetu, watembee kulinda ujambazi na amani itokee lakini hata magari na matairi yao ya magari hayana uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine hata service zenyewe na hata namna wenyewe wanavyoweza kujikimu na hata kulala kwenye majanga kwenye maeneo mengine. Kwa kweli naomba na Waziri wa Fedha namwona yuko hapa na Kamati ya Bajeti mko hapa nawaomba wizara hii hebu iangalieni kwa jicho la pekee kwa sababu fedha zinazotengwa hazilingani na kazi wanayoifanya na ugumu wa kazi waliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia magari ya zima moto ni magari ya zamani yamechoka. Juzi mliona moto hapa Dodoma unatokea hayafanyi kazi sawasawa wanaunulieni magari ya kisasa, tunaona kabisa Serikali imenunua magari nchi nzima imepeleka karibu Ma-OCD wote wana magari. Lakini hata matairi ni yale mapya yaliyokuja nayo hata mafuta ya kuweka kwenye hayo magari hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba jamani hebu tupigie kelele Serikali yetu na najua Serikali yetu ni sikivu na Rais wetu amekuwa mstari wa mbele kulinda vyombo vyetu hivi kama ambavyo anavyofanya kwenye majeshi na vyombo vya ulinzi na usalama jeshi la polisi, magereza, zimamoto watendewe haki kwa kuongezewa bajeti na hata fedha waliotengewa mwaka jana yote iende kama ambavyo imekusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nimejielekeza kuongelea maslahi ya askari, hata anayezungumza na mimi na maslahi na askari. Familia yote ya Mzee Makilagi tuko watoto 24 mimi peke yangu ndio raia na mimi niliponea chupuchupu. Kwa hiyo, nachozungumza hapa nazungumza tukiwa ndani ninaomba nitoe ushauri askari wetu wote wa polisi magereza, zima moto, uhamiaji wanafanya kazi ngumu katika mazingira magumu. Ninaomba sisi kama Bunge hebu tuielekeze Serikali tujaribu hata kuwaongezea mishahara na hasa askari wa kiwango cha chini. Mishahara yao ni ya zamani kwa kweli haiendani na mazingira ya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile askari wetu wanafanya kazi kwenye mazingira magumu, posho zao za kujikimu, posho zao za likizo, posho zao za uhamisho hawapati. Askari anakwenda kila baada ya miaka mitatu anakwenda likizo lakini sasa hivi hata nauli wakati mwingine wanajitegemea tunapeleka wapi jeshi, tunawasaidiaje hawa vijana wetu ambao ndio walinzi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuangalie kwa macho ya huruma kwa sababu askari tumewaambia wasichukue rushwa, askari huyu hana muda hata wa kufanya biashara, hana muda wa kukaa wa kufanya mambo yake binafsi muda wote anatulinda sisi, sasa anapokwenda mpaka likizo anajitegemea kwa kweli sio sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie posho zao. Posho zao tunamshukuru Rais wetu na hata Awamu ya Nne, na hata Awamu ya Tano wanapata posho kujikimu ya chakula kila tarehe 15 wanapata shilingi 300,000.

Sasa hivi umekuja utaratibu eti wanapewa kila mwezi ninaomba ule utaratibu wa kupewa kila tarehe 15 ya kila mwezi wawe wanapewa kwa sababu ile tarehe 15 anapopata ile fedha inawasaidia kupunguza zile changamato ndio maana hawatakwenda kukamata huko ndio maana hawatajiingiza kwenye mambo mabaya lakinii unapolimbikiza mpaka mwisho wa mwezi sio nzuri. Ninaomba tuwaongeze pia kwa sababu tangu tulipowaongeza ilikuwa ni mwaka 2010 sasa ni 2015 tuwaongeze askari wetu toka hii 300, 000 ifike hata ikiwezekana 500,000 kwa sababu wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilitaka nizungumzie ni ma…

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, na ninataka nimshauri Mheshimiwa Kangi tena nafurahi kwa sababu wewe…

MWENYEKITI: ngoja

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nani kanipa taarifa huyo nani alete.

MWENYEKITI: Subiri kidogo taarifa.

T A A R I F A

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba pamoja na kwamba anasema askari wanapewa posho lakini yeye alikuwa miongoni mwa Wabunge waliokataa maaskari kuongezewa mshahara hapa Bungeni na wafanyakazi wote kwa ujumla. Kwa hiyo, ni taarifa tu kwamba anapozungumzia hilo akumbuke kwamba alikataa wafanyakazi kupandishiwa mishahara na maaskari wakiwa ni miongoni mwa wafanyakazi katika nchi hii. (Makofi)

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Makilagi

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya huwa siongeagi na watoto nimekusikia, kwa hiyo, ataongea na size yake mimi sio size yake. Mimi naongea na baba yako umesikia mwanangu eeh!

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kwa kusema kwamba askari wetu tuangalie maslahi yao kwa sababu wanalinda Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tuzungumzie maslahi ya askari, vitendea kazi sasa hivi ipo changamoto kwa uniform za askari na sio kwa jeshi la polisi peke yake mpaka zimamoto, magereza, ukikutana na askari sio kama yule wa zamani uniform zake zinatofautiana. Ninaomba kwenye fedha za OC kwa ajili ya shughuli mbalimbali hebu tuongeze bajeti hii ili vyombo vyetu vya Serikali viweze kununua uniform…(Makofi)

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumza nao wanasema wakati mwingine hata wanaambiwa wanunue wao wenyewe.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Selasini kuhusu utaratibu kanuni ya ngapi.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba utaratibu kwa mujibu wa kanuni ya 64(1)(g) mzungumzaji wakati anajibu taarifa alisema kwamba haongei na watoto. Sasa licha ya kwamba hii sio kauli ya kibunge lakini kama kiongozi wa Kambi hii siongozi watoto, ninaongoza Wabunge, watu wazima na watoto wamebaki nyumbani. Sasa i baba yao ninaomba ieleweke hivyo… (Kicheko)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Makilagi endelea.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa sababu Mbunge anayezungumza ndio baba mwenyewe ninayemzungumza tutakaa pamoja kuwalea watoto kwa pamoja. Na ndio jukumu letu sisi kama wazazi ndani ya Bunge hili kuwalea watoto ili wazazi wanapokuwa wanazungumza watoto wanakuwa na utulivu na wanaweka heshima kwa wazazi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maslahi ya askari, leo nimesema najielekeza kwenye maslahi ya askari wetu, Rais wetu anawapenda askari kila anapopita mnamwona anawapenda askari na alipokwenda Arusha mwaka jana alitoa shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kujenga nyumba za askari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa mujibu wa taarifa ya waziri nyumba zinaendelea kujengwa na baadhi yake nimezitembelea kwa kweli nichukue nafasi hii kumshukuru Rais kwa kazi njema. Ushauri wangu katika jambo hili pamoja na kazi nzuri ya kutenga hizo fedha bilioni kumi nataka nimwambie Mheshimiwa Kangi tena ambaye ni askari na wewe hebu sasa njoo na mkakati wa kujenga nyumba za askari za kutosha kwa nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushauri kila unapofanya ziara usiache kutembelea kambini fika na pale feed force Mkoa wa Mara, fika na pale Mwanza Mabatini, fika na hapa Dodoma uone askari wako mahala wanapolala. Ninaomba mje na mkakati maalum na sisi Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na sisi Wabunge wa CCM tuko wengi na wengi tunapenda askari tuko tayari kupitisha mpango huu ili nyumba za askari zijengwe nchi mzima na zilete tija kwa askari wetu walale mahala pazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nawashauri pia hata ramani ya nyumba za askari ziangaliwe tena kwa sababu nyumba zilizojengwa zamani zilikuwa ni kwa ajili ya familia ambazo hazina watoto, sasa hivi askari wetu wanaishi vizuri wana watoto vile vinyumba haviwastahili hebu njooni na ramani ambayo inavutia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Waziri kuna kitengo cha ujenzi kwa upande wa magereza na kwa upande wa polisi. Sifurahii kuona kuna kazi imetokea jeshi la polisi, kazi wanapewa jeshi la wananchi, sifurahii kama mtoto wa askari kwa sababu nimeshiriki kujenga handaki, nimeshiriki kujenga hata nyumba za askari. Zamani familia za askari tukishirikiana na magereza, tukishirikiana na kitengo cha ujenzi tulikuwa tunajenga nyumba wenyewe. Hiki kitengo kimekwenda wapi? Na bahati nzuri jeshi la polisi lina wataalam waliobobea katika weledi wa ujenzi, lina Ma- engineer, lina wachoraji, lina kila kitu, mageraza ina rasilimali watu, Mheshimiwa Waziri hebu sasa uache legacy katika nchi hii. (Makofi)

MWENYEKITI: Asante sana Mheshimiwa Makilagi.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana naunga mkono hoja (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naomba nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu na nikushukuru wewe kwa kuniwezesha kusimama na kuweza kutoa mchango wangu katika sekta hii muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuunga mkono hoja hii iliyo mbele yetu. Naiunga mkono kwa sababu Wizara ya hii ya Elimu ukilinganisha na tulipotoka kazi kubwa na nzuri inafanyika katika sekta hii. Naomba kabisa nimpongeze Waziri Mheshimiwa Prof. Ndalichako; Naibu Waziri, Mheshimiwa Olenasha; Katibu Mkuu na watendaji wake na timu nzima ya Wizara ya Elimu kwa kazi njema na kubwa mnayoifanya ya kuhakikisha sekta ya elimu sasa inaleta tija kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Mheshimiwa Prof. Ndalichako Mungu akubariki sana, ni mama usiyejikweza, unafanya makubwa ukisaidiana na wenzako. Leo wakati unawasilisha ulikuwa unatuonyesha kwenye picha, kwa kweli umetushangaza, tumeona maghorofa yanavyojengwa mikoani mpaka Nyasa na maeneo mengine. Wote huo ni ubunifu wako pamoja na watendaji wenzako, mimi na wenzangu tunakuunga mkono. Niungane na Mheshimiwa Rais alipokuwa kule Mtwara alitamka bayana kwamba anafurahishwa na kazi yenu, chapeni kazi na muendelee kusonga mbele, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba asitokee mtu yeyote kuwakatisha tamaa kwa sababu Waswahili wanasema vizuri vyajiuza na vibaya vyajitembeza. Maana watu wamezoea akifanya kidogo kashatoka kwenye media siyo Mheshimiwa Prof. Ndalichako na wenzake, wanafanya vitu vikubwa vinajitangaza vyenyewe. Hongereni sana, endeleeni kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane na maoni ya Kamati yangu ya Huduma za Jamii. Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa hapa Serikali inafanya kazi nzuri sana ya kupeleka fedha katika sekta hii. Unaona fedha ya miradi ya maendeleo karibu asilimia sitini na kitu imekwenda, OC zaidi ya 37%, mishahara ni karibu 100%. Hata hivyo, naomba niungane na maoni ya Kamati kusema kwamba fedha inayopelekwa hailingani na kazi ya sekta hii. Naomba niishauri Serikali na Waziri wa Fedha kama yupo anisikilize, sekta hii naomba ipelekewe fedha 100% kama iliyopangwa ili miradi ya maendeleo itekelezwe na fedha za OC siweze kufanya kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya ziara sisi kama wana Kamati, tumetembelea chuo cha DUCE tumeona kazi nzuri sana iliyofanywa na Serikali, fedha zaidi ya shilingi milioni 500 zimekwenda. Ukiangalia kuanzia taarifa ya Waziri na ya Kamati fedha zilizotengwa hazikwenda zote matokeo yake mradi hakuna kinachoendelea. Tumekwenda Chuo cha Mwalimu Nyerere pale Kigamboni, kuna fedha iliyotengwa kwa ajili ya mradi mpaka tunakwenda kukagua hakuna fedha iliyokuwa imekwenda. Naomba sana na bahati nzuri Waziri wakati tunaongea nawe kwenye Kamati ulituhakikishia kwamba kwa sababu bado miezi inaendelea itatafutwa fedha na kupelekwa, naomba nami nisisitize hilo kwa sababu hii ni fedha ambayo tulitenga kwenye bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha ya OC ndiyo inakwenda kulipa Wahadhiri wetu. Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa na tulizozipata tena kupitia kwa Wenyeviti wa Bodi, Wahadhiri wetu wana madai yao ya kodi ya nyumba. Mhadhiri ni kiongozi, ni mtumishi, ameaminiwa, anafanya kazi kubwa lakini hana uhakika wa kuishi. Naiomba Serikali yangu Tukufu na sikivu hebu pelekeni hizi fedha za OC ziende kulipa madeni ikiwepo na fedha za watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba nitoe ushauri, kazi nzuri tuliyoiona pale Mwalimu Nyerere na DUCE kupitia vyanzo vya ndani wameweza kujenga miundombinu. Naomba nitoe ushauri, vyuo vingine na kama ambavyo Kamati tumesema igeni mfano wa vyuo hivi, kwa sababu vyanzo vya mapato vya ndani vipo lakini wakati mwingine havitumiki vizuri wote tunasubiri Serikali Kuu. Naomba tuwaige hawe DUCE na Mwalimu Nyerere ili na vyuo vingine viweze kutengeneza miundombinu kwa kutumia vyanzo vya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nivishauri vyuo vyote nchini vikiwepo vyuo vikuu na vyuo vya ufundi kubuni vyanzo vingine vya mapato. Sisi kwenye Kamati tuliona kuna uwezekano wa kubuni ambavyo vitafanya vyuo vijiendeshe bila kutegemea ruzuku kutoka Serikali Kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye Chuo cha Julius Kambarage Nyerere cha Sayansi ya Kilimo ambacho kwa mujibu wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambaye na mimi ni mdau niliyeshiriki kuiandika na kutafuta maoni ya wananchi, tulipofika Mkoa wa Mara na kwa Watanzania walituambia wanataka mawazo ya Mwalimu yatimie. Mwalimu Nyerere na wenzake walitoa eneo bure kwa Serikali, walijinyima wakatoa zaidi ya heka karibu 450 kwa ajili ya kujenga chuo. Mwalimu Nyerere akajenga miundombinu ikiwemo Bwawa la Kialando, bwawa la mfano ili kesho na kesho kutwa kijengwe chuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chuo hiki kiliwekwa kwenye Ilani, ukurasa wa 101, Ibara ya 52, kifungu cha K, kifungu cha pili kidogo kinaeleza bayana kwamba, endapo CCM itachaguliwa 2015 – 2020, Chuo cha Mwalimu Nyerere Butiama kitajengwa. Nimefurahishwa na kazi inayoendelea kwa ajili ya ujenzi wa chuo hiki. Tumeona mipango kwa ajili ya kutafuta hati miliki.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Okay.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nilitaka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba kwenye ukurasa katika Chuo kilichozungumzwa hapa cha Mwalimu Nyerere kinachozungumzwa pale ni kwamba Chuo kijiandae kufundisha wajasiriamali kiangalie watu wanaokamua na kuangalia kuku, sio kufundisha wanafunzi waliokuwepo hapa. Kwa hiyo, mambo mengine yaliyoandikwa humu ni kwamba nataka kumpa taarifa kwamba aendelee kuona kwamba hiki Chuo ni muhimu sana na wanaohusika wakione kama Chuo cha Mwalimu Nyerere sio kwenda kufundisha kuku. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, taarifa naipokea kwa sababu Mbunge Getere ni Mbunge mwenzangu wa Mkoa wa Mara, na hivi karibuni tulikuwa kwenye kikao cha RCC. Moja ya agenda zetu ilikuwa pia ni kuzungumzia Chuo cha Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapongeza kwa haya yaliyofanyika, nimeona mmehangaika kutafuta hatimiliki, sasa tunataka tujue hivi mmeishia wapi, kwa sababu, suala la upatikanaji wa hatimiliki hata kwa mtu wa kawaida. Siku hizi kwa sababu Serikali ya CCM imerahisisha miundombinu, na tumeletewa Ofisi iko katika Kanda ambayo Ofisi yetu iko Simiyu wiki mbili unapata hati. Inakuwaje leo Chuo cha Mwalimu mpaka leo hati haijapatikana, changamoto ni nini? Tunapongeza mambo yanayofanyika kuna maandiko yameandikwa, kuna mafunzo yanaendelea pale kwa ajili ya kuanzisha hiki Chuo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijue Mheshimiwa Prof. Ndalichako mama ninaye kuamini, na mama ninaye kupenda, na kwenye Kamati pia nilikuuliza kwenye Randama yako nimeona umetenga bilioni moja, nilitaka nijue ni za nini?. Nataka kujua hizi fedha kwa ajili ya kujenga Chuo, na hasa kwa kuzingatia kwamba tunaelekea mwaka 2020 mwisho wa Ilani hii ya CCM ambayo tuliiahidi kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua fedha kwa ajili ya ujenzi wa Chuo hiki, ziko wapi? Na ningependa kujua chuo kinaanza lini? Kwa sababu Serikali imeshawekeza, Mbunge wetu mpendwa, Mzee wetu, Mzee Mkono na Mungu ampe Wepesi apone, arudi Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amejitahidi kujenga majengo na akayatoa bure kwa Serikali ilikuwa ni shule ya High School tukawaondoa watoto, majengo yapo na pa kuanzia palikuwepo kuna Chuo cha Kisangwa ambacho tulisema itakuwa ni sehemu ya Chuo Kikuu kile. Kuna maeneo ya Chuo cha Bweri, maeneo ya kule Rorya, tulisema yote yatakuwa ni sehemu ya Chuo, wakati tukijiandaa kujenga miundombinu. Ningependa kujua hivi Mheshimiwa Waziri, Mkakati ni nini kutekeleza ndoto za Mwalimu alizozitoa akiwa hai, na kama kweli tuna lengo la kumuenzi Baba wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua Mheshimiwa Waziri na timu yako, hivi ninyi mnaonaje, mmeshaajiri wafanyakazi tena wenye weledi, yuko Profesa pale Mkuu wa Chuo, mpaka amestaafu yule anayekaimu sasa ndiyo amekuwa Mkuu wa Chuo. Analipwa mshahara pamoja na watendaji wenzake zaidi ya kumi na nne, leo hakuna kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda Mheshimiwa Waziri, hebu utakaposimama hapa, Watiama, narudia tena Watiama, akiwemo Baba wa Taifa aliyetangulia mbele ya haki. Ninapozungumza Watiama naongelea Wazanaki wa Butiama, walio kuwa na dhamira hiyo ya kujenga Chuo, wanataka leo wakusikie kauli yako, Chuo kitajengwa na Chuo kitafunguliwa na lini, ndiyo walichotuma leo nilete hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie ujenzi wa miundombinu ya shule ninapongeza sana Serikali yangu Tukufu ya Chama cha Mapinduzi, imefanya kazi nzuri ya kujenga miundombinu ikiwemo Vyuo vikuu na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kama mama…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, liko tatizo Mheshimiwa Waziri kwenye suala la miundombinu na hasa katika mabweni katika Vyuo Vikuu watoto wetu wa kike wanakaa katika maisha…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa,

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wanapanga kwenye majumba matokeo yake wanakuwa ni wake wanaolewa na watu.

MWENYEKITI: Muda wangu sio rafiki.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wanakosa kodi za kulipa wanatembea masafa marefu…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, na hata Vyuo vya Dar es Salaam kwenda kutafuta hiyo huduma. (Makofi)

MWENYEKITI: Muda wangu sio rafiki.

MBUNGE FULANI: Naam…

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Mheshimiwa Waziri Ndalichako utakapokuja hapa..

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Baba alikuwa anatoa taarifa huku.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mmejipangaje, kujenga miundombinu kwa ajili ya hosteli ya wasichana, Chuo cha DUCE, Chuo cha Mwalimu Nyerere, Chuo cha Ardhi na Vyuo vyote nchini tumejiandaaje ili kuwanusuru watoto wetu wa kike ambao wanaingia kwenye dhahama ya kulipa kodi kiwango ambacho ni kigumu, na sio kwa watoto wa kike peke yake…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Makilagi.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naongelea na VETA, kuna VETA hapa zinajengwa nchini naomba na Kisangwa iliyoko Mkoa wa Mara hebu ipe kipaumbele kwa sababu majengo pia yapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kuweza kusimama na kutoa mchango wangu katika bajeti hii muhimu ambayo ni bajeti ya maji, bajeti ambayo kwa kweli ndiyo uhai wa Taifa letu. Kwa kweli maji ni uhai na bila maji hakuna chochote ambacho kinaweza kufanyika ikiwemo hata masuala ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuleta salam za wananchi ninaowawakilisha ambao ni wanawake wa Tanzania walionipitisha kwa kura zao zote za kishindo tena kura zote za ndiyo. Wamenileta nilete salamu; wale wananchi wanaotoka katika maeneo yaliyopata maji kwa asilimia 64 wanaishukuru Serikali kwa kazi njema waliyoifanya ya kujenga miundombinu. Hao ni wale wa vijijini wamenituma nije niishukuru Serikali yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naleta salamu za wananchi wanaoishi maeneo ya mjini na hasa katika Makao Makuu ya Mikoa kwa kiwango cha maji kwao sasa ni asilimia 80. Wanawake hawa wamenituma nije kusema ahsante sana maana Serikali imewatendea haki. Vile vile wapo wanawake walionituma wanaoishi katika miji midogo midogo, kwa kiwango cha asilimia 64 wamepatiwa maji safi na salama na wenyewe wanasema ahsante. Hata maandiko ya dini yanasema, mtu anayeshukuru huwa anaomba tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilete salamu za wanawake wa Tanzania, kama alivyosema Mheshimiwa Kitandula, bado kuna Watanzania zaidi ya 20,000 hawapati maji. Wanawake ambao nawawakilisha ambao wamekuwa wakitembea kwa umbali mrefu, ambao wamekuwa hata hawafanyi kazi wanashinda barabarani, ambao wamekuwa hata hawapati nafasi ya kukaa na familia, kulea familia zao, kila wakati wako barabarani na wenyewe wamesema nilete kilio chao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake wanaomba Serikali yao Tukufu, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Magufuli, ambapo kwa kweli ni wanawake wa Tanzania, wanawake wa nchi hii, ambao ndio walioiweka madarakani, wanaomba Serikali ithubutu, itafute fedha na hata kama ni za kukopa na kama ni kuongeza vyanzo vya mapato kwenye kodi ya mafuta, kwenye mitandao ya simu na namna yoyote ile wanavyoona inafaa, fedha zitafutwe kwa ajili ya kupeleka maji vijijini, wanawake wa Tanzania waweze kuhudumiwa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamenituma niseme wanawake wamevumilia kwa muda mrefu sana, wanapata adha kubwa sana. Kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi tumewaahidi kuwatua ndoo ya maji kichwani. Hebu Serikali yetu na tunajua inaweza ikathubutu, itafute hizi fedha kwa namna inavyojua na kwa vyovyote vile miradi itekelezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilete salamu za wananchi wa Mkoa wa Mara. Tunashukuru sana kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa leo, tumeona kuna miradi mingi inakwenda kutekelezwa katika Mji wa Mugumu. Katika ile Miji 29 na Mugumu ni wadau. Tunaomba tulete shukurani zetu, ahsante Serikali kwa kisikiliza kilio cha Wana-Mara, Mji wa Mugumu sasa upate maji safi na salama. Ni kwa muda mrefu wananchi wa Mji wa Mugumu wamekuwa wakitumia maji kama tope. Tunaishukuru Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunaishukuru sana Serikali inakwenda kujenga mradi wa maji Tarime ambapo kwa muda mrefu sana tumekuwa tukileta kilio. Naomba kwa niaba ya wananchi wa Tarime, Majimbo yote mawili; Tarime Mjini na Tarime Vijijini nilete shukurani zao kwa mradi unaokwenda kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naleta shukurani kwa wananchi wa Rorya na hasa wananchi wa Mji wa Shirati, Mji ambao ni mkongwe, Mji ambao umekuwepo miaka mingi. Wananchi wanazungukwa na ziwa lakini kwa muda mrefu wamekuwa hawapati maji. Kwa awamu hii sasa naona Serikali inakwenda kuwatendea haki. Kwa kweli kipekee nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wako, tumeona ambavyo mmekuwa mkifuatilia katika Mkoa wetu kuhakikisha wananchi wa Mkoa wa Mara wanapata maji kwa sababu ni haki yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mara unazungukwa na Ziwa Victoria, Mto Mara, Mto Suguti na Mto Simiyu, lakini kiwango cha upatikanaji wa maji Mkoa wa Mara kwa vijijini ni kwa kiwango cha asilimia 50.8 na kwa upande wa mjini ni asilimia 60. Kwa hiyo, bado naona kwa kweli hali ni mbaya. Ni imani yangu na ni imani ya Wabunge wa Mkoa wa Mara na wananchi wa Mkoa wa Mara na hasa wanawake, miradi hii ikienda kutekelezwa tena kwa wakati itaongeza kiwango kikubwa cha maji na wanawake wa Mkoa huu wataachana na adha hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie mradi wa Mgango-Kyabakali - Butiama mradi ambao nimeusikiliza kwa muda mrefu sana, tangu Mbunge akiwa Marehemu Dkt. Magoti, Mwenyezi Mungu amjaalie. Akaondoka, akaja Balozi Ndobo, ameupigia kelele katika Bunge ameondoka; amekuja Mheshimiwa Mkono, vipindi vyote viwili ameupigia kelele, hakuna kilichofanyika; amekuja Profesa Muhongo; nami tangu nimeingia Bunge hili, Awamu ya Kwanza nilikuwa Mjumbe wa Kamati ya Maji, tumeupigia kelele, kila jibu tunalopewa, mradi utajengwa kupitia BADEA, mradi utajengwa kupitia Saudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013, Serikali ya Tanzania ilisaini mkataba na BADEA, ilisaini mkataba na Saudia na tukakubaliana kwamba ifikapo 2015 mradi utakamilika. Nimefurahishwa kwenye kitabu hiki nimeona mradi unaendelea na mipango nimeiona ni mizuri na ninaona mambo ni mazuri. Naomba Mheshimiwa Mbarawa ambaye umekuwa ukiniambia hata huko nje na Mheshimiwa Muhongo hata juzi mlikaa naye, hebu wewe tuambie wananchi wa Mgango na Butiama wanapata maji au hawapati? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mradi unaanza lini? Kwa sababu kusema kweli nimepitia vitabu vya hotuba nyingi, kila wakati inazungumzwa BADEA lakini mradi hauanzi. Mheshimiwa Waziri alipokuja na Mheshimiwa Rais alituambia mradi tunakwenda kutangaza tenda na siyo muda mrefu mradi utaanza. Leo tunakwenda kumaliza mwaka, napenda leo tusikilize kauli yake, atakapokuja kuhitimisha hii hoja, wananchi wa Mgango wanamsubiri, wananchi wa Butiama nyumbani kwa Baba wa Taifa wanamsubiri, akina Mzee Msuguri waliotumikia nchi kwa uaminifu na weledi mkubwa wakapumzika, wanahaingaika na maji. Jamani hamwoni aibu ndugu zangu tupige kelele kila siku? Hebu Mheshimiwa Waziri tuambieni mkakati ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoshituka hapa, naona huu mradi kwa kiwango kikubwa unategemea fedha za nje, BADEA na Saudia, nafikiri ndiyo maana hautekelezeki. Leo Mheshimiwa Mbarawa nakupongeza kwa sababu umeweka fedha nyingi zaidi ya shilingi bilioni nane kwa fedha za ndani. Nitoe ushauri kwako, nami najua ni Waziri msikivu ambaye umekuwa ukitusikiliza Wabunge na umesikiliza Watanzania wote; hebu hizi shilingi bilioni nane, ni fedha nyingi, mradi basi uanze hata wananchi wawe na matumaini ili Saudia na hao BADEA watakapokuja, watukute tuko barabarani. Kusema kweli tumeshaongea kule maneno yote yamekwisha. Kila wakati, wananchi wanapoteza imani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Mheshimiwa Waziri mwenyewe alipokuja Butiama siku ile na Mheshimiwa Rais alipoelezea huu mradi kama alikuwa anafuatilia, wananchi walinyamaza kimya kwa sababu viongozi wengi walishawaambia hivyo. Alianza Mheshimiwa Dkt. Shukuru Kawambwa aliwaambia hivyo, hakuna kitu; akaja yule Mheshimiwa Profesa Mwandosya, hakuna kitu; akaja Mheshimiwa Profesa Maghembe, tena yeye alikwenda kabisa mpaka kwenye chanzo na tuliongozana naye, hakuna kitu; amekuja juzi Mheshimiwa Engineer Lwenge hakuna kitu. Kwa hiyo, hata yeye alipokuwa akiwaambia siku ile mbele ya Mheshimiwa Rais, walikuwa wanaona hakuna kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu leo Mheshimiwa Waziri toa neno la matumaini kwa wananchi wa Wilaya ya Butiama, nyumbani kwa Baba wa Taifa, kuliko na kaburi, tusiendelee kuomba maji hapa hata kwa ajili ya kumiminia lile kaburi lake kumwagilia maua Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie upatikanaji wa fedha. Mwaka 2018 Serikali ilitenga fedha nyingi sana, lakini kwa mujibu wa Bajeti hii fedha hazikutoka zote. Nami naungana na wenzangu kwamba fedha sasa zitole. Lipo tatizo kubwa ambalo naliona, hawa Wakandarasi ambao wanawazungumza wenzangu, kwa kweli baadhi ya maeneo Wakandarasi ni wa ovyo sana. Hawana uwezo, wengine sio waaminifu, wengine wamefikia hatua wanakimbia miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu fanyeni tathmini, hivi tunao Mainjinia wa miradi ya maji? Kwa sababu Tanzania naona tunazalisha Mainjinia nchini na wengi hawana kazi wako majumbani, hivi kweli…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri; na Waziri amekusikia.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia lakini vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu, Mungu muweza wa yote aliyenipa fursa hii ya kuweza kusimama na kuweza kuzungumza jioni hii katika Bunge lako Tukufu. Naomba nianze kwa kuunga mkono hoja hii iliyo mbele yetu hoja ambayo ni muhimu kwa ustawi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono na sababu ninazo. Sababu ya kwanza Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango, Naibu Waziri, Katibu Mkuu wote na timu yake yote ya Wizara ya Fedha na Watendaji wote na Mawaziri na Serikali chini ya uongozi wa mpendwa wetu Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli wamefanya kazi nzuri katika bajeti iliyopita. Nimejaribu kupitia vitabu vyote hivi, nimeanzia na kitabu cha hotuba ya Waziri, nimepitia Taarifa ya Hali ya Uchumi katika Taifa, nimepitia kitabu cha Mpango wa Utekelezaji wa Bajeti, wanyonge wanyongeni haki yao wapewe kazi wamefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono bajeti hii kwa sababu hata bajeti iliyopita kwa kiwango kikubwa ilijielekeza katika miradi ya kufufua uchumi wa Taifa letu. Huwezi kusema unataka kufikia uchumi wa kati bila kuwa na reli yenye viwango vya kimataifa, huwezi kusema unafikia uchumi wa kimataifa bila kuwa na ndege za kutosha kwa ajili ya utalii na kwa ajili ya uchumi. Huwezi kufikia viwango vya kimataifa bila kuwa na umeme wa uhakika, bila kuwa na kilimo chenye tija, hizo ndizo sababu zangu za kuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono kwa sababu Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2019/2020, umelenga kutekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi na umelenga kwenda kutekeleza malengo endelevu. Katika yale malengo endelevu yote Serikali ya Tanzania imeweka vipaumbele tisa na vyote vipo katika mpango, sina kila sababu ya kuunga mkono bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono kwa sababu kero zote zilizokuwa ni kero kwa ajili ya uchumi wa Taifa letu zimeondolewa, Mungu atupe nini, ninaunga mkono. Ninaunga mkono bajeti hii kwa sababu vipaumbele vyote vilivyowekwa vinalenga utashi wa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tazania. Ukienda kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa 16 umejieleza vema, Mheshimiwa Rais alipoingia alituonesha kabisa anataka kuingia kwenye uchumi wa kati na bajeti hii imezingatia matakwa ya Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya utangulizi huo, naomba sasa nijielekeze katika mambo machache na leo nimechagua kwa sababu Wabunge wengi wameshaongea kabisa wiki nzima hii mengi wameshayagusia. Leo nimeona nijielekeze katika maeneo yanayogusa wananchi walinichagua na si wengine ni wanawake wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao kwa kweli katika kuchangia pato la Taifa wao ndiyo wanaoongoza katika Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo taarifa zinaonesha uchumi wa Taifa letu kwa kiwango kikubwa pia unategemea kilimo. Wazalishaji kati ya asilimia 65 wanawake ni zaidi ya asilimia 80 wanalima na kwa bahati mbaya wanalima kwa kilimo cha mkono. Wanawake wa Tanzania ndiyo tunaotegemea katika kilimo hata akina baba watanisapoti, ukipita huko vijijini watu unaowakuta kwenye mashamba ni wanawake na watoto wao wa kike. Akina baba walio wengi wanalima lakini si kwa kiwango cha wanawake. Nikitolea Mkoa wetu wa Mara na hasa walaya ninayotoka wanawake ndiyo wanaolisha hata familia, wanawake ndiyo wanaolea familia, wanawake ndiyo wanaoleta uchumi wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa leo nimeona nijielekeze kuwasemea katika kilimo na hapa ndipo waliponituma. Kilimo chao bado kinategemea jembe la mkono, kilimo chao bado kinategemea kilimo kisichokuwa na utaalam, kilimo chao bado kinategemea kutokuwa na pembejeo za kutosha, kilimo chao bado hata kupata fursa zenyewe za kupata mikopo kwa ajili ya kununua pembejeo bado, kilimo chao hata mazao wanayolima bado kuwa na uhakika wa masoko bado.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona leo nije niishauri Serikali, kama kweli tunataka kufika uchumi wa viwanda na kuipeleka Tanzania katika uchumi wa kati ninaishauri Serikali yangu tukufu hebu tuwekeze kwenye kilimo. Hapa ninatoa ushauri kwamba ni lazima Serikali katika bajeti hii na hata katika bajeti zijazo tujielekeze kuimarisha kilimo chetu na katika vipaumbele vyetu kama ambavyo bajeti imesema, tuongeze wigo wa kilimo cha umwagiliaji. Tanzania ina hekta nyingi sana za kilimo, zaidi ya 4,000 lakini zinazofanyiwa kilimo ni chache sana. Mpango wa Wizara ya Maji kwa mwaka uliopita walielekeza wanataka tufikie hekta 1,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kwamba Serikali iharakishe hii mipango ili twende kwenye kilimo cha umwagiliaji. Hatuwezi kujikomboa kiuchumi kama bado tunaendelea kutegemea kilimo cha mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya mikoa, kwa mfano hii Kanda ya Kati ya Dodoma hata ufanyeje, kuna Wilaya kama ya Kongwa hata ukilima mazao kama ya mahindi hayaoti. Ukienda Mkoani kwetu Mara sasahivi ardhi imechoka. Sasa tunayo maziwa, mito, maji ya mvua na mpaka hatuna hata mabwawa. Ninaishauri Serikali hebu sasa tutafute fedha kwa ajili ya kuwekeza katika kilimo ili sasa uchumi wetu huu tunaouzungumza kwamba umekuwa kwa kiwango cha asilimia 7.5 sasa uende hata kumnufaisha mwananchi ili naye aone matokeo ya kukua kwa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee uwezeshaji wa wanawake kiuhumi. Ninaipongeza Seriakli yetu ya Chama cha Mapinduzi, imekuwa mstari wa mbele kuwawezesha wanawake. Kama ambavyo nimetangulia kusema, mwanamke ndiye kila kitu, ukimuwezesha mwanamke ni sawasawa na kuliwezesha taifa. Ni ukweli usiopingika kwamba mapato anayoyapata mwanamke kwa kiwango cha asilimia zaidi ya 90 kinakwenda kwenye familia. Ninaposema hivi ninao ushahidi kwa sababu akina baba matumizi yao ni mengi, lakini hakuna mama anayeweza akaishi vizuri bila kuhakikisha mtoto wake anasoma bila kuhakikisha malezi ya mtoto. Hawa akina baba wakipata hela zinakuwa na matumizi mengi lakini akina mama akikipata vyote vinakwenda kwenye familia. Kwa hiyo ninashauri hapa, hebu tuwawezeshe wanawake kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mwaka wa fedha uliopita 2016/2017 tulitengeneza hapa sheria ambayo inaitaka Serikali kila palipo na jambo lolote la manunuzi, kila mahali ambapo wanatengeneza tender, iwe ni kujenga barabara, reli na kufanya kila kitu katika miradi ya maendeleo asilimia 70 wanaopata hiyo kazi au wanaopata hiyo zabuni au wanaopata hiyo tender wawe ni wanawake. Ninafurahia mpango huo na ninaipongeza sana Serikali yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kufanya utafiti, baadi ya taasisi zetu za Serikali hazitekelezi. kKwa hiyo ningependa kujua Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa hebu tuambie, tangu tumepitisha sheria hii mpaka sasa ni wanawake wangapi wananufaika? Na kama hawanufaiki Serikali ina mkakati gani? Kwa sababu baadhi ya miradi ni mikubwa, kwa mfano mradi wa ujenzi wa Stiegler’s Gorge, mradi wa reli na miradi mingine hata ya kununua ndege wanawake wananufaikaje? Tujue! Hata hivyo, hata huko kwenye kilimo hata kwenye miradi mingine ya ujenzi wa madarasa, n.k tujue wanawake wananufaikaje. Tunapoagiza vitu kutoka nje ya nchi wanawake kwenye asilimia 30 wananufaikaje. Hapa nitaomba Mheshimiwa Waziri utakapokuaj hebu tusaidie kuainisha ili baadaye sisi kama Bunge tupime, isije baadaye sheria hiyo nayo ikaja ikaondolewa kwa sababu tumeshindwa kusimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naona wenzangu walikuwa wanapiga kelele juu ya mambo ya taulo za kike. Taulo za kike tulijichelewesha wenyewe, tulifanya uzembe, sisi wenyewe Wabunge hatukuwa serious, matokeo yake mpaka imeondoka. Sasa na kwenye hili naomba tusiwe wazembe, hii asilimia 30 tunasemaje katika kuhakikisha inanufaisha wanawake?…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imegonga Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. AMINA S. MAKILAGI: Nitaleta kwa maandishi ikiwemo pamoja na taulo za kike nimetoa ushauri wangu, nimezungumzia juu ya asilimia tano ya wanawake, vijana na walemavu na nimezungumzia pia utaratibu wa utoaji wa uboreshaji wa mapato ya kodi. Nitaleta kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kukushukuru wewe na kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote kwa kunipa fursa ya kusimama na kutoa mchango wangu katika sekta hii muhimu ya maji ambayo ndiyo uhai wa mwanadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja; na sababu zangu za kuunga mkono hoja hii ni kama zifuatazo:-

Kwanza, taarifa ya Waziri juu ya utekelezaji wa kazi zilizofanyika mwaka 2016/2017 na mpango wa utekelezaji wa kazi kwa mwaka wa fedha 2017/2018 imeandaliwa vizuri na hasa kilichonivutia ni taarifa ya hatua iliyofikiwa ya kila mradi wa maji ukiachilia mbali ile miradi michache iliyosahaulika.

Pili, naunga mkono kwa kuwa Serikali ya CCM chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais - Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Mheshimiwa Majaliwa K. Majaliwa, wanaonesha kwa vitendo dhamira ya CCM na dhamira ya Mheshimiwa Rais ya kuwatua wanawake ndoo kichwani. Pamoja na pongezi, naomba nijielekeze kutoa ushauri kwa Serikali katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuishukuru Serikali kwa kupeleka fedha za maendeleo, bado Serikali haijapeleka fedha za kutosha katika miradi ya maendeleo. Hadi Machi, 2017 Serikali ilikuwa imepeleka shilingi bilioni 181.2 sawa na asilimia 19.8 tu. Ni ukweli usiopingika kuwa upelekaji wa fedha za miradi ya maendeleo uko chini sana, hivyo utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya maji unakwama kwa sababu hakuna fedha za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali, kama kweli ina dhamira ya kuwatua ndoo wanawake kichwani, basi ni lazima Serikali ihakikishe kuwa inapeleka fedha zote zilizotengwa kwenye bajeti kwa ajili ya miradi ya maji iliyopangwa kwa mwaka wa fedha husika. Hapa
nashauri, fedha ambazo hazijapelekwa zipelekwe sasa kabla ya mwaka huu wa fedha 2016/2017 kwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono pendekezo la Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji la kuongeza sh.100/= ya kila lita ya petroli na dizeli. Natoa ushauri huu kwa sababu tozo ya sh.50/= ya dizeli na petroli inayotolewa sasa imeleta matokeo mazuri sana ya miradi ya maji. Hivyo, tukiongeza tozo ikawa sh.100/=, kasi ya ujenzi wa miradi ya maji itaongezeka na dhamira ya Mheshimiwa Rais na CCM ya kuwatua ndoo wanawake kichwani itatekelezwa na wanawake wataachana na adha wanayopata ya kutembea masafa marefu kwenda kutafuta maji badala ya kufanya kazi zitakazowakomboa kijamii na kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia fedha zitakazopatikana kutokana na tozo zipelekwe mapema katika miradi ya maji iliyopo vijijini ili kuwatua akinamama ambao hasa ndio wanaoathirika zaidi na shida ya kukosa maji. Katika kitabu cha maoni ya Kamati ukurasa wa 15 inaonesha kuwa asilimia 46 tu ya wakazi wa vijijini ndiyo wanapata maji safi na salama. Kwa hiyo, fedha za tozo kwenye mafuta zielekezwe kusaidia upatikanaji wa maji vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwashukuru Serikali na BADEA na SFD kwa mpango uliopo wa kutekeleza Mradi wa Mugango na Kiabakari (Butiama) kwa Dola za Kimarekani 30.69 ingawa mradi huu mpaka sasa haujaanza kutekelezwa. Pamoja na kuishukuru Serikali na Wadau kwa hatua zinazoendelea za kumpata Mkandarasi na kupeleka taarifa hizo BADEA kwa ajili ya kupata kibali cha ujenzi unaotarajiwa kuanza mwaka 2017/2018. Hapa naomba niseme kwamba, mradi huo umechukua muda mrefu kuanza, kiasi kwamba wananchi wanakaribia kukata tamaa juu ya mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali kwa Serikali; kwa kuwa mpango wa mradi huu ni wa muda mrefu na mpaka sasa wananchi wanaelekea kukata tamaa na mradi huu, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie hawa wadau wetu wa maendeleo watatoa lini hicho kibali na mradi uweze kuanza ili wananchi zaidi ya 80,000 waweze kupata maji safi na salama? Je, kama wadau wetu hawako tayari kutoa fedha hizi, Serikali ina mpango gani juu ya kutoa fedha ili mradi uanze bila kutegemea fedha za wafadhili?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Mradi wa Maji – Mji wa Musoma, naishukuru Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Ufaransa kwa kuboresha huduma ya maji safi na salama katika Manispaa ya Musoma kwa gharama ya shilingi bilioni 45 ambapo mradi unalenga kuongeza uzalishaji wa maji kutoka lita milioni 10.14 za sasa hadi kufikia lita milioni 34 kwa siku ambazo zitakidhi mahitaji ya wananchi wa Musoma hadi mwaka 2025 na utekelezaji wa mradi umefikia kiwango cha asilimia 90. Tunashukuru sana. Pamoja na shukrani hizi, naomba kushauri yafuatayo juu ya mradi huu:-

(i) Ijengwe miundombinu ya maji ili wananchi waliopo kwenye chanzo cha maji cha Kata ya Etaro, Nyigina wapate maji kutokana na chanzo hiki; na

(ii) Pia kwa kuwa matenki ya maji yanaweza kuhifadhi maji mengi, nashauri ijengwe miundombinu itakayopeleka maji haya Kata ya Nyakanga, Bukabwa na Butiama kwa kuwa wataalam wa mradi huo wanasema inawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kujenga miundombinu ya maji katika mradi wa Dar es Salaam na Pwani. Naipongeza DAWASA na DAWASCO kwa kusimamia mradi huu kwa kiwango cha hali ya juu. Pamoja na pongezi hizi, naishauri Serikali ihakikishe mradi huu unawanufaisha wananchi wa Mkoa wa Pwani, Kisarawe, Mkuranga, Bagamoyo na Kibaha kwa sababu vyanzo vya maji vya miradi hii viko Mkuranga na Kibaha na matenki ya maji yamejengwa Kisarawe.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa Bwawa la Kidunda ni wa muda mrefu takriban miaka 20 mradi haujaanza. Napenda kujua Serikali ina mkakati gani ili kuhakikisha mradi wa ujenzi wa Bwawa la Kidunda unaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu uvunaji wa maji ya mvua na kilimo cha umwagiliaji. Napenda kuishauri Serikali kupitia Wizara ya Maji ije na mpango wa kuvuna maji kwa kujenga mabwawa ya kuhifadhi maji hasa katika Mikoa ya Kanda ya Kati kama vile Singida, Dodoma na Shinyanga. Uvunaji wa maji ya mvua utasaidia kukuza kilimo cha umwagiliaji hapa nchini hasa katika mikoa ambayo imekuwa haipati mvua za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, katika Mkoa wa Dodoma kumekuwa na ongezeko kubwa la watumishi kuhamia Dodoma ambapo zaidi ya watumishi 2000 wamehamia Dodoma huku chanzo cha maji kikiwa ni kile kile cha Mzakwe. Sambamba na hilo ujenzi wa mabwawa kama vile bwawa la Farkwa umekuwa ukisuasua. Katika mwaka 2017/2018, Serikali iendelee kufanya utafiti ili kupata vyanzo vipya vya maji ili kukabiliana na tatizo la upatikanaji wa maji nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kilimo cha umwagiliaji bado kuna changamoto ya kupeleka fedha katika miradi ya umwagiliaji. Katika kitabu cha maoni ya Kamati inaonesha kuwa Serikali ilipeleka asilimia tatu tu kwa mwaka 2002, lakini kwa mwaka 2003 na 2004 Serikali haikupeleka hata shilingi moja pamoja na kuwa bajeti ya umwagiliaji ilitengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nianze kwa kukushukuru wewe na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kuweza kusimamia na kutoa machango wangu katika hoja hii muhimu ya Hali ya Uchumi wa Taifa, Taarifa ya Utekelezaji wa Bajeti Iliyopita pamoja na Mapendekezo ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Mwaka wa Fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja kwa sababu zifuatazo;

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na viambatisho vyake imeandaliwa vizuri sana kwa sababu imejielekeza kwa uwazi kabisa wapi tulipotoka wapi tulipo katika kutekeleza ilani ya CCM 2015 na utekelezaji wa Mpango wa Taifa uliozingatia pia Mpango wa Maendeleo Endelevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono kwa kuwa katika mwaka huu wa fedha tunaomaliza kesho kutwa Serikali imefanya kazi nzuri ya kukusanya mapato, kudhibiti mapato, yaliyokuwa yakipotea pamoja na kupeleka fedha katika miradi ya maendeleo. Mwaka huu kila mkoa umepata fedha nyingi ukilinganisha na miaka mingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono kwa sababu bajeti hii imegusa maeneo yote ambayo Mheshimiwa Rais ameyawekea mkazo tangu achaguliwe; Mheshimiwa Waziri ameeleza vizuri sana kupitia hotuba yake ukurasa wa 16.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono kwa sababu bajeti ya 2019/2020 imepunguza utegemezi kwa kiwango kikubwa. Naunga mkno kwa sababu kodi zote zaidi 54 zilizokuwa vikwazo katika kukuza uchumi zimeondolewa. Naunga mkono kwa sababu vipumbele vilivyowekwa vinalenga kukuza uchumi wa taifa na kutoa huduma kwa wananchi waliotuchagua. Naunga mkono kwa kuwa bajeti hii 2019/2020 ni bajeti ya matumaini.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo haya naomba nijielekeze katika maeneo machache niliyoyachagua kuyatilia mkazo ambayo yanagusa wananchi ninaowawakilisha ambao ni wanawake wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ambao walio wengi ni wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kuhusu Kilimo. Zaidi ya Watanzania 65 wanaotajwa kujihusisha na kilimo asilimia 80 ni wanawake ambao wanalima kilimo cha kujikimu tu, kilimo cha kutegemea mvua, kilimo cha jembe la mkono, kilimo bila utaalamu, mbegu duni, kilimo ambacho mazao yao hayajaongezewa thamani na mazao yao kukosa soko na kukosa mitaji ya kuwekeza katika kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu; pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya kuhakikisha kilimo chetu kinaleta tija kwa wanawake, wananchi na taifa kwa ujumla naomba kushauri yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuwaondoa wanawake katika kilimo cha jembe la mkono na kutumia nyenzo za kisasa, kama vile majembe ya kukokotwa na ng’ombe, matrekta pamoja na kupatikana tena kwa pembejeo za kilimo na kwa wakati; na hapa benki ya kilimo ihusike kikamilifu kwa sababu lengo la kuanzisha benki hii lilikuwa ni kuwakomboa wakulima wanyonge ambao wengi wao ni wanawake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kilimo cha umwagiliaji Serikali kwa kushirikiana na Sekta binafsi iongeze wigo wa kujenga miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji kutoka hekta 475.052 hadi kufikia hekta 1,000.000, ikiwa ni hatua muhimu ya kutekeleza mpango ulioandaliwa na Wizara ya Maji 2018/2019. Kwa kutekeleza mpango huu kilimo chetu kitakuwa ni kilimo chenye kuleta tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kuongeza wataalam wa kilimo na kuwawezesha watekeleze wajibu wao kikamilifu. Serikali ipeleke pembejeo za kilimo tena kwa wakati. Serikali kuhakikisha inawawezesha wanawake na wananchi kupata masoko ya mazao ya ndani na nje. Serikali ihakikishe kunakuwepo na viwanda vya kusindika mazao ya wakulima. Serikali iwawezeshe wanawake mitaji ya kutosha katika sekta ya kilimo ili waweze kuanzisha miradi mikubwa. Serikali itoe elimu kwa wakulima juu ya kilimo bora ili wanawake na wananchi waweze kuzalisha mazao yenye viwango vyenye ubora.

Mheshimiwa Naibu Spika, Uwezeshaji wa Wanawake Kiuchumi. Pamoja na kwamba wanawake ndio wazalishaji wakubwa, wanawake pia ndio walezi wa familia, wanawake ndio hata wanapopata kipato walio wengi kipato hicho hukielekeza katika familia zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuipongeza Serikali kwa kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia fursa mbalimbali, bado wanawake walio wengi ni masikini na hata wanachokizalisha hawanufaiki nacho.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Manunuzi. Swali; Bunge tulipitisha Sheria ya Manunuzi iliyoweka kifungu kwamba kila manunuzi yatakayofanyika au tenda zitakazotolewa asilimia 30 zielekezwe kwa wanawake. Pia tumepitisha sheria ya kuzitaka kila halmashauri kutenga asilimia 10 kwa ajili ya kuwezesha vikundi vya kiuchumi. Pamoja na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri hiyo bado lipo tatizo la baadhi ya taasisi hizi kutekeleza Sheria ya Manunuzi kwa kiwango cha asilimia 70 kama ilivyoainishwa kwenye sheria baadhi ya halmashauri zinashindwa kutekeleza sheria ya kutoa asilimia 10 ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Vilevile mchango wa wanawake unaotolewa katika kulea familia haujathamanishwa katika kukuza uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali; ningependa kujua tangu sheria hii imeanzishwa wanawake wangapi wamenufaika na Sheria hii ya Manunuzi na katika maendeleo? Ni ujenzi wa barabara, ujenzi wa reli nakadhalika. Swali tumepitisha sheria ya kutenga asilimia 10 ya wanawake na vijana na watu wenye ulemavu. Tangu sheria hii imepitishwa ya kila halmashauri kutenga asimilia 10 ya mapato yake ya ndani ni wanawake wangapi wamenufaika ukilinganisha na kabla ya sheria haijarekebishwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali; wanawake wengi wameanzisha vikundi vya kiuchumi; tatizo lao kubwa ni kukosa mitaji, hii ni kwa sababu baadhi ya halmashauri mapato yao yako chini hivyo vikundi havipati mikopo ya kutosha ya kuweka misingi imara ya kiuchumi. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzisaidia halmashauri kuongeza vyanzo vya mapato na kufanya uwekezaji wa kilimo cha umwagiliaji katika halmashauri nyingi zinazotegemea mapato yanayotokana na kilimo cha kutegemea mvua? Zikiwemo halmashauri za Musoma Vijijini, na Butiama kupitia Bonde la Bugema na Mto Mara?

Mheshimiwa Naibu Spika, Huduma ya Maji kwa Wanawake na Wananchi Katika Kuchangia Uchumi wa Taifa. Kama nilivyotangulia kusema kuwa wazalishaji wetu wakubwa katika taifa ni wanawake. Wanawake walio wengi wanashindwa kufanya kazi za uzalishaji mali kutokana na tatizo la maji. Ushauri; Serikali iendelee kutafuta fedha kwa ajili ya kuwekeza katika miradi ya maji ili kuwawezesha wanawake kuacha kutembea umbali mrefu kwenda kutafuta maji na badala yake washiriki kufanya kazi zitakazowakomboa kiuchumi. Ushauri; kwa kuwa kwa mujibu wa taarifa ya Mheshimiwa Waziri deni la Taifa linahimilika, Serikali iendelee kutafuta mikopo na fedha za ndani kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji. Huduma hii ya maji ikiboredhwa itawakomboa wanawake ambao ndio wazalishaji wakubwa na itachochea uchumi wa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Upotevu wa Fedha za Miradi ya Maji. Fedha za miradi ya maji zimekuwa zikipotea na miradi kutokamilika kwa sababu za usanifu mbaya wa miradi hiyo na kupewa kandarasi wasio na sifa. Swali; ningependa kujua, je, Serikali imejipangaje kupata wataalamu wa kusanifu miradi na wakandarasi wenye uwezo wa kujenga na kusimamia miradi ya maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mchango wa Wanawake Unaotolewa Katika Kulea Familia. Wanawake wamekuwa mstari wa mbele katika kulea familia. Je, ningependa kujua kama mchango wa wanawake umethaminiwa na kuingizwa katika mchango wa taifa wa kukuza uchumi? Nimeomba kujua kwa sababu wanawake walio wengi wanatoa mchango katika kulea familia lakini kwa bahati mbaya mchango wao haujathaminika; hivyo, wamenituma niulize, je, Serikali inautambua?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukusanyaji wa mapato pamoja na kuipongeza Serikali kwa kukusanya mapato na kuiwezesha Serikali kutekeleza malengo yake ikiwa ni pamoja na kuliona mishahara na kutekeleza miradi ya maendeleo ni na ushauri kidogo katika eneo hili. Serikali iendelee kufuatilia kwa karibu mianya yote ya upotevu wa mapato katika bandari, uwanja wa ndege, bandari bubu, bandari kavu, mipakani pamoja na kwenye manunuzi ya umma hasa katika miradi ya maendeleo nakadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, taulo za watoto wa kike. Nashauri Serikali iwezeshe wanawake wajenge viwanda vidogo vya kuzalisha taulo za kike na kutoa bei elekezi. Fedha inayopelekwa halmashauri kwa ajili ya maelekezo ya kununua taulo za kike ipelekwe kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naomba nianze kwa kukushukuru wewe na Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama na kutoa mchango wangu katika sekta ambayo, ili kuendelea katika mambo manane, ardhi ndiyo ya kwanza; bila kuwa na ardhi hatuwezi kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja kwa sababu nne (4) zifuatazo:-

Kwanza, kitabu cha hotuba kimeandaliwa vizuri sana, maneno machache, takwimu kwa wingi.

Pili, Mheshimiwa Waziri William Lukuvi, Naibu Waziri Mheshimiwa Angelina Mabula, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na timu yake, wanafanya kazi nzuri sana ya (kupigiwa mfano). Ni ukweli usiopingika kuwa, watendaji walio wengi wa Wizara ya Ardhi wamebadilika, hongereni sana, ongezeni bidii zaidi ili muwakomboe Watanzania hasa wanawake.

Tatu, mipango ya kusikiliza kero za wananchi; naunga mkono kwa sasa, Wizara imeweka mipango mizuri ya kutatua kero za wananchi kupitia Mabaraza ya Ardhi, Mahakama za Ardhi, Ofisi za Wakuu wa Wilaya na Mikoa na Halmashauri za Wilaya.

Nne, Hati zilizofutwa/kurudishwa kwa wananchi; naunga mkono kwa sababu Serikali imefuta baadhi ya hati ambazo zilimilikiwa na watu wachache kwa muda mrefu bila kuendelezwa na kurudishwa kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ushauri ninayo mambo ya kuishauri Serikali katika, sehemu chache nilizochagua kuzitilia mkazo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, mpangilio wa Matumizi ya Ardhi, Wanawake na kumiliki Ardhi, pamoja na kuishukuru Serikali kwa kuhakikisha wanawake na wanaume wanapata fursa, katika umiliki wa ardhi kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi ya Kijiji ya 1979 kifungu cha (4-5). Katika kutoa nafasi ya umiliki wa ardhi kwa akinamama bado taratibu za kimila hazitoi fursa kwa wanawake hasa wa vijijini kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri, Serikali itazame upya taratibu za kimila kwa kuzifanyia marekebisho ili kutoa fursa kwa akinamama kumiliki ardhi. Ningependa Waziri atakapokuja hapa kuhitimisha Hotuba yake atuambie na wanawake wasikie kwamba, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha taratibu za kimila ambazo ni kandamizi zinazowanyima wanawake fursa ya kumiliki ardhi sambamba na wanaume zinaondolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, migogoro ya wakulima na wafugaji, hifadhi na wananchi; pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya kutatua migogoro ya ardhi, bado tatizo ni kubwa. Ushauri wangu, Serikali itafute fedha ya kupima ardhi yote ya Tanzania. Ni muhimu sasa Serikali Kuu itafute fedha hata kwa njia ya mkopo kwa ajili ya kupima ardhi yote ya Tanzania na kupanga matumizi bora ya ardhi. Kila eneo lipangiwe matumizi yake ili kuondoa migogoro ya wakulima na wafugaji ambayo imekuwa ikigharimu maisha ya Watanzania wengi. (Suala la kupima ardhi lisiachwe kwa Halmashauri iwe ni ajenda ya Kitaifa).

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, utoaji wa Hati za Viwanja; pamoja na kazi nzuri ya utoaji wa hati kwa wakati, bado wananchi wanaotumia ardhi karibu asilima 80 hawana hati miliki. Mfano; katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali iliahidi kutoa hati miliki za ardhi 400,000 lakini hadi kufikia tarehe15 Mei, 2017, Serikali ilikuwa imetoa hatimiliki 33,979 tu, sawa na asilimia 8.5 ya lengo zima (ukurasa 18). Kiwango hiki ni kidogo sana ukilinganisha na uhitaji wa hatimiliki hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri, Serikali iweke mipango itakayohakikisha wananchi wote wanaotumia ardhi wanapata hati miliki. Matokeo ya mipango hii ni kwamba, viwanja vya wananchi vitawaletea tija kwa kutumia hati zao kufikia fursa za kiuchumi. Pia Serikali itapata mapato ya uhakika; sasa wananchi watakuwa wanalipia kwa mujibu wa sheria (kodi ya kila mwaka). Swali langu, je, Serikali imejipangaje kwa mwaka 2017/2018, kuhakikisha lengo la utoaji wa hati miliki ili kuendana na kasi ya ongezeko la idadi ya watu na mifugo inafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, Mipango Miji; pamoja na kuipongeza Serikali kwa kuhakikisha Miji na Majiji yanapangwa. Naomba niishauri Serikali, kuhakikisha Miji yote inakuwa na master plan ili kuondoa tatizo la kuwa miji holela ambayo haikupangwa halafu baadaye tunapotaka kujenga miundo mbinu tunalazimika kuhamisha wananchi waliojenga kabla ya miji kupimwa na kusababisha hasara kwa Serikali, kulipa fidia pia ujenzi wa miundombinu ya maji, umeme na zinapotokea ajali za moto tunashindwa kuwafikia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, Ujenzi wa Nyumba unaofanywa na National Housing na Kampuni ya Watumishi Housing: Pamoja na kulipongeza Shirika la Nyumba na Kampuni ya Watumishi Housing kwa kujenga nyumba na kuwakopesha wananchi. Swali langu ni kwamba, je Mashirika haya yana mkakati gani wa kujenga nyumba za bei nafuu zaidi ambazo wananchi wengi hasa watumishi wa umma wa kipato cha chini wataweza kumudu kununua? Ujenzi wa nyumba za milioni 40 bado hii ni gharama kubwa sana kwa Watanzania ambao bado ni maskini hasa wale wanaoishi vijijini na wafanyakazi wenye kipato cha chini hasa wanawake ambao ndio walezi wa familia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya, Mabaraza ya ardhi na Nyumba ya Wilaya bado hayapo kwenye wilaya nyingi. Kwa hiyo, wananchi wengi wanakosa haki zao kutokana na mabaraza haya kutokuwepo. Pia utengenezwe utaratibu wa kuendesha kesi ambao ni rahisi kwa wananchi kuweza kuandika maandiko juu ya matatizo hayo. Nauliza, Serikali ina mpango gani kuhakikisha mabaraza haya yanakuwepo katika kila Halmashauri/Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, saba, Kodi ya majengo kwa sasa inakusanywa na TRA, Serikali iweke utaratibu mzuri wa TRA kuwafikia wananchi au kushuka kwa wananchi ili kukusanya kodi hizi na aidha, Serikali ifanye tathmini kwa kiasi gani imeweza kukusanya mapato yanayotokana na kodi ya majengo ili kuona kama kuna mafanikio mara baada ya kazi hii kukabidhiwa TRA badala ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nane ni kuhusu mashine za kufyatua matofali. Pamoja na shukrani nyingi kwa Shirika la Nyumba la Taifa chini ya Mkurugenzi Ndugu Mchechu, kutoa mikopo ya mashine za kufyatua matofali kwa vikundi vya vijana katika Halmashauri. Je, Shirika la Nyumba la Taifa limejipangaje kwa mwaka 2017/2018 kuhakikisha kuwa mikopo ya mashine za kufyatua matofali inatolewa kwa vikundi vya akinamama ili kuweza kujipatia kipato na kujenga nyumba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niungane na wenzangu kuchangia hoja iliyo mbele yetu. Kwa kuwa leo nina dakika tano, nitaenda kwa haraka kama ifuatavyo; Mungu anisaidie niweze kuzitumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ya kwanza naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kuweza kunipa afya. Namshukuru yeye kwa sababu bila yeye nisingeweza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa uthubutu wake na kwa dhamira yake na kuhakikisha sekta ya afya inakwenda kuleta tija kwa wananchi kwa kuhakikisha anapeleka fedha za dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika nchi yetu ni 5% zinakwenda kwa wananchi. Kwa utayari wake sasa, Mheshimiwa Rais wetu anaboresha vituo vya afya, hospitali za wilaya na hospitali za rufaa. Nani kama Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoweza kusema ni kwamba awasamehe ambao hawajui watendalo, kwa sababu waswahili wanasema, akutukanaye hakuchagulii tusi. Ukiwa kwenye maji unaoga, akija mwendawazimu, humfukuzi. Hata waliosema kuna fedha zilipotea na wenyewe pia awasamehe kwa sababu leo ufafanuzi umetolewa mzuri na ninaomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya utangulizi huo, namshukuru sana Waziri na timu yake. Mwenyewe Mheshimiwa Ummy na Katibu Mkuu. Kusema kweli unapoona mambo mazuri, ujue kuna Watendaji na viongozi wazuri. Taarifa imeandaliwa vizuri na kazi inaendelea vizuri, hongera sana. Endeleeni kuchapa kazi, nchi yetu iweze kufika pale tunapohitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niungane na Mheshimiwa Agness Marwa kuleta shukrani za wananchi wa Mkoa wa Mara kwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kujenga Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara, Mwalimu Nyerere Memorial Centre. Hospitali hii kwa muda mrefu tangu ukoloni imejengwa kwa nguvu za wananchi. Wananchi wa Mkoa wa Mara walichanga fedha nyingi na kilikuwa ni kilio cha muda mrefu. Kwa uongozi wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, sasa hospitali inajengwa na fedha zinakuja. Tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachokiomba sasa aendelee kutenga fedha, mahesabu yameshafanyika, zinahitajika shilingi bilioni 24. Fedha zipelekwe ili Hospitali ya Rufaa Memorial kwa ajili ya wananchi wa Mkoa wa Mara iweze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninasema hivyo kwa sababu katika Kanda ya Ziwa Hospitali ya Bugando imelemewa. Hospitali ya Bugando inahudumia mikoa zaidi ya tisa. Population ya watu kwa mujibu wa sensa ni watu zaidi ya shilingi milioni 15 ni pamoja na Kanda ya Magharibi. Hospitali ya Bugando inapokea watu wa ugonjwa wa kansa. Kwa mujibu wa utafiti uliofanyika Kanda ya Ziwa ndiyo watu wanaathirika sana. Hospitali ya Bugando kwa siku inapokea wagonjwa zaidi ya 50 kwa siku wanaokuja kwa ajili ya mionzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Bugando haina hospitali hata ya kulaza wagonjwa wa kansa. Pamoja na kuishukuru Serikali kwa kuboresha Hospitali yetu ya Bugando ambayo inahudumia wananchi wa Kanda ya Ziwa wakiwemo na wa Magharibi na hata wa nje ya nchi, ninaomba sasa fedha zipelekwe ili hiki kituo cha kulaza wagonjwa wa kansa kiweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naishukuru sana Serikali kwa kupeleka fedha kwa ajili ya kujenga vituo vya afya hapa nchini. Ni ukweli usiopingika kwamba kazi imefanyika vizuri, ushauri wangu sasa, katika bajeti inayoendelea na itakayokuja baadae, ninatoa ushauri kwa sababu nimekuwa nikitembea nchi nzima, ninaomba muwe mnaangalia na maeneo ya pembezoni. Mfano, Wilaya ya Nyasa, Wilaya mpya, ina kituo kimoja cha afya cha Serikali. Wananchi wote wanahudumiwa pale. Hospitali ile haina hata gari la kubeba wagonjwa na vilevile Wilaya ya Nyasa haina hata barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mtakapokuwa mkipeleka magari ya kubebea wagonjwa na hata kupeleka vipaumbele vya hizi fedha kwa ajili ya kujenga Hospitali za Wilaya, na Vituo vya Afya, angalieni hapa ikiwemo na Musoma Vijijini imekuwa ni Wilaya ambayo imekuwa inaitii sana Serikali. Tumejenga shule nyingi kwa nguvu za wananchi, kuanzia msingi mpaka lenta; kila kata tumejenga. Sasa kwenye wilaya kama hizi ambazo tulijielekeza kwenye elimu, nilikuwa naomba na kwenye vituo vya afya, hebu angalieni na Musoma Vijijini. Tuna Kituo kimoja cha Mlangi ambacho kinahudumia kama Wilaya nzima ya Halmashauri ya Musoma. Musoma ina Hospitali ya Rufaa, lakini population ya watu wamekuwa ni wengi, haiwezi kuhudumia katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie upungufu wa wataalam katika sekta ya afya. Kwa mujibu wa taarifa zilizowasilishwa, hali ni mbaya. Madaktari hasa mabingwa hakuna, hata huko Bugando kuna upungufu mkubwa sana. Hata Hospitali ya Mkoa wa Mara tuna madaktari wawili tu. Siyo Mara peke yake kwa sababu, mimi Jimbo langu ni Tanzania nzima. Katika hospitali zote nilizozitembelea na hata Vwawa juzi nilikuwa Mbozi, hali ni mbaya. Tunaomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya kuwapeleka wataalam katika hospitali zetu na hasa Madaktari Bingwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nitoe ushauri, nendeni mkaongee na Watanzania walioko Botswana. Mimi nilishaanza kufanya nao mazungumzo; wako tayari kurudi nyumbani kwa manufaa ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, muda ni mfupi, naomba kuunga mkono na mambo mengine nitayaleta kwa maandishi. (Makofi)

Mhesimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama na kutoa mchango katika hoja hii muhimu ya maji na uhai.

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi, nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa sekta hii ya maji na umwagiliaji kwa kazi nzuri waliyofanya kuandaa randama na hotuba hii na kuiwasilisha vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawapongeza Waziri na timu yake kwa jinsi wanavyojituma kufuatilia kero za maji na kuzipatia ufumbuzi. Hakika ninaungana na nukuu ya usemi wa Mzee Makamba kwamba; “ujana siyo sifa na uzee siyo sifa, sifa ni hapa kuna kazi nani anaiweza.” Hongera sana Waziri pamoja na umri wako kazi ya sekta hii unaiweza na umefanya vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kujenga miundombinu ya maji mijini na vijijini kwa kiasi kupunguza tatizo la maji hasa mijini ukiwemo na mradi mkubwa wa kupeleka maji katika Jiji la Dar es Salaam na miji mingine hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizi, nashauri zitengwe fedha kwa ajili ya kujenga miundombinu ya maji katika Jiji la Dar es Salaam na katika miji mingine ili kuondoa tatizo la upotevu wa maji na mradi wa maji wa visima vya Mpera, Kimbiji na Ruvu ili uwanufaishe wananchi wa Mkoa wa Pwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Miradi ya Maji Vijijini iliyofadhiliwa na Benki ya Dunia pamoja na kuipongeza Serikali, Benki ya Dunia kwa kutafuta fedha na kujenga miundombinu ya miradi ya maji katika vijiji na katika kila Halmashauri za Wilaya na kuwezesha wananchi/wanawake kuondokana na kero ya maji. Pamoja na pongezi hizi, miradi ya maji ya vijiji kumi katika baadhi ya Halmashauri za Wilaya haikusimamiwa vizuri na baadhi ya miradi haikukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali, ningependa kujua:-

(i) Ni vijiji vingapi miradi imekamilika na wananchi wanapata maji na katika Halmashauri zipi?

(ii) Ni miradi mingapi imekamilika lakini maji hayatoki na nijue tatizo ni nini na ufumbuzi wake ni nini?

(iii) Miradi mingapi iko katika hatua za ujenzi na itakamilika lini na iko katika Halmashauri ya Wilaya gani na itakamilika lini?

(iv) Je, Serikali imejipangaje katika kuhakikisha miradi ambayo ilikamilika na haitoi maji inatoa maji na miundombinu ya miradi ambayo haijakamilika. Nini mipango ya kukamilisha miradi hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Mugango wa Kiabakari Butiama, mradi wa kujenga miundombinu Mugango - Kiabakari - Butiama ni mradi ambao ulipangwa kutekelezwa miaka mingi zaidi wakati wa Waziri wa Maji Ndugu Mwandosya, tangu wakati huo hadi sasa maelezo ni kwamba mradi huo utajengwa kwa fedha za wadau BADEA na kwamba zimekwishapatikana USD 32.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa miundombinu ya kupeleka maji mpaka Butiama kwenye kaburi la Baba wa Taifa kwa kweli limekuwa ni jambo linalotia simanzi kubwa sana kwa wananchi wa Wilaya ya Butiama kwa sababu mradi huu hautekelezwi kama ulivyopangwa. Swali:-

(a) Ningependa kujua hivi tatizo hasa ni nini mbona ujenzi wa mradi huo hauanzi?

(b) Je, fedha hizo kutoka BADEA USD 32 zipo na ziko katika akaunti gani na zimeingia lini?

(c) Mkandarasi aliyeteuliwa kujenga miundombinu ya maji ya mradi huu wa Mgango - Kiabakari - Butiana ni nani na anaanza kazi lini?

(d) Ningependa kujua pia kama mradi huu utakamilika utawahudumia pia wananchi Kata ya Buruma, Butuguli na Muliyaza kwa sababu mradi huu miundombinu yake itapita katika baadhi ya vijiji vya kata hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri, ningependa kujua kama mradi huu utawahudumia wananchi wa Kata ya Mgango, Kiriba na Tegeruka maeneo ambayo yako karibu sana na chanzo cha Mradi wa Maji cha Mgango.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa miundombinu ya maji katika maeneo yanayozungukwa na maziwa na mito; pamoja na kuipongeza Serikali kwa kujenga miundombinu ya maji katika vyanzo vya maji ya maziwa na mito mfano, Ziwa Victoria linatoa maji mpaka Tabora na Wilaya zake. Ningependa tutumie fursa ya mito na maziwa kujenga miundombinu ya maji katika:-

(a) Mkoa wa Mara unazungukwa na Ziwa Victoria, Mto Mara na Mto Sisiti.

(b) Mkoa wa Mwanza tupeleke maji katika Wilaya zote kwa kutumia maji ya Ziwa Victoria na Mto Sibiti.
(c) Mkoa wa Geita - Ziwa Victoria.

(d) Mkoa wa Simiyu – Ziwa Victoria na Mto Simiyu.

(e) Mkoa wa Kagera – Ziwa Victoria, Mto Kagera na mito mingine.

(f) Mkoa wa Ruvuma – Ziwa Nyasa Mkoa wa Ruvuma, Mbeya, Songwe na Ruvuma na Mkoa wa Katavi na Kigoma tutumie Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ijengwe miundombinu ya maji katika mikoa ya Pwani, Dar es Salaam, Lindi, Tanga, Mto Rufiji utosheleze maji katika Mkoa wa Pwani, Dar es Salaam na Lindi. Mikoa ya Morogoro na Mto Kilombero, Mkoa wa Dodoma Mto wa Mtera na Mto Zigi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo cha umwagiliaji, pamoja na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri ya kujenga miundombinu ya umwagiliaji, naishauri Serikali yafuatayo:-

(a) Kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji ili kuongeza kiwango cha uzalishaji wa chakula na biashara hasa katika maeneo ambayo hayapati mvua za kutosha. Pia tuwe na uhakika wa chakula bila kutegemea mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa kilimo Bugwema Irrigation ningependa kujua:-

(a) Bugwema Irrigation inamilikiwa na nani?

(b) Je, kuna mkakati gani kuhakikisha mradi huu unafufuliwa na unaleta tija kwa wananchi wa Musoma Vijijini na Mkoa wa Mara na Taifa kwa ujumla na hasa Wilaya ya Musoma Vijijini, Butiama, Bunda na Wilaya ambazo zimekuwa zikikumbwa na ukame. Vilevile ardhi kuchoka na pia kuna ugonjwa wa mihogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Manispaa ya Musoma pamoja na kuipongeza Serikali kwa kujenga miundombinu ya maji na kuwawezesha wananchi kuweza kupata maji kwa kiwango kikubwa ijengwe miundombinu kwa ajili ya kufikisha maji katika vijiji vya Kata ya Nyakanga, Bukabwa Wilaya ya Butiama na Kata ambazo ziko karibu sana na chanzo cha maji Musoma Mjini na miundombinu iliyojengwa ikiboreshwa kidogo inaweza kufika huko. Pia nashauri mradi huu ufikishe maji katika vijiji vya Bukanga Kata ya Etalo, Kata ya Rifulifu, Nyegina na Nyakatende Wilaya ya Musoma Vijijini kwa sababu wako karibu na chanzo cha maji yanayokwenda Musoma Mjini. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote kwa kuniwezesha kusimama na kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Waziri na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Makamanda Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama kwa kuandaa hotuba nzuri na Waziri kuiwasilisha vizuri. Nampongeza Waziri na Watendaji wote kwa kuhakikisha hali ya ulinzi na usalama wa raia na mali zao unaimarika siku hadi siku, kudhibiti dawa za kulevya, kudhibiti uhamiaji haramu na kukabiliana na majanga ya moto nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na kuipongeza Serikali kwa kupeleka fedha kwa ajili ya shughuli za kawaida na shughuli za maendeleo na kufikia kiwango cha asilimia 78 bado tatizo la upelekaji wa fedha za kutosha katika sekta ya Mambo ya Ndani jambo ambalo linasababisha kushindwa kutekeleza kikamilifu wajibu wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kupitia Wizara ya Fedha kuingalia Wizara hii nyeti ya Mambo ya Ndani kwa jicho la pekee na kuwapelekea fedha kama zinavyopitishwa na Bunge kwa sababu kutofanya hivyo wanashindwa kutengeneza magari, kununua vipuri vya magari, kununua mafuta ya magari na kununua vitendea kazi muhimu kama magari na hasa magari ya zimamoto. Mfano, Makao Makuu hapa Dodoma magari ya zimamoto yapo mawili ambapo moja lipo uwanja wa ndege na lingine ndilo linalotegemewa katika Mkoa mzima wa Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya ujenzi wa nyumba za Askari na vituo vya Polisi; pamoja na kuipongeza Serikali kwa ujenzi wa makazi na vituo vya Polisi na pia kumpongeza Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, tarehe 7 Aprili, 2018 wakati akizindua nyumba za Askari Mkoani Arusha alitoa shilingi bilioni kumi kwa ajili ya ujenzi wa makazi ya Askari ngazi ya chini, ambapo fedha hiyo itasaidia kujenga nyumba 400 katika mikoa yote nchini, tunamshukuru Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni Jeshi la Polisi na Magereza wafufue Kitengo cha Ujenzi ambacho kipo na kilikuwa kikifanya vizuri sana kwa sababu, kinao wataalam ambao kwa sasa wamepangiwa kazi katika maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivyo kutasaidia kujenga nyumba nyingi za Askari Polisi, Magereza, Uhamiaji na Zimamoto, tena kwa wakati na kwa haraka na kuokoa fedha nyingi, kwa sababu Jeshi letu la Magereza litatoa nguvu kazi. Serikali ipeleke fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Askari Polisi, Magereza, Uhamiaji na Zimamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna nyumba za Askari zilizojengwa katika Mkoa wa Mara na Mwanza hazitumiki, ningependa kujua ni lini zitatumika? Pia, ningependa kujua kuna majengo na ofisi zimejengwa, lakini hazijakamilika, ningependa kujua mkakati wa kukamilisha majengo hayo na katika bajeti hii ni fedha ngapi zimetengwa kwa ajili ya kuyakamilisha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, maslahi ya Askari wetu, utaratibu wa upandishaji wa vyeo; pamoja na kupongeza majeshi yetu ya vyombo vya ulinzi na usalama na kuwa na utaratibu wa kanuni ya ajira na upandishaji wa madaraja, bado yapo malalamiko kwa baadhi ya Askari wetu na hasa waliokaa kwa muda mrefu ambao wamefanya kazi kwa uaminifu na uadilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa upandishaji wa vyeo haukuzingatia muda wa mtu alivyokaa kazini, bali unazingatia elimu aliyonayo. Nashauri kauni hii itazamwe upya ili kuwapa askari waliofanya kazi kwa muda mrefu, kwa weledi, uaminifu na uadilifu mkubwa ili na wao wapewe kipaumbele katika kuwaongezea madaraka na hasa kwa kuzingatia kwamba majeshi haya yanawategemea watumishi wa kada hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupandishwa vyeo bila kurekebishiwa mishahara; lipo tatizo la askari kuongezewa madaraka bila kurekebishiwa mishahara, jambo linaloathiri ufanisi. Vilevile Askari anapostaafu anajikuta amepata fedha ambayo hailingani na madaraka aliyonayo, ningependa kujua hapa tatizo ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo pia la baadhi ya Askari wanaostaafu kucheleweshewa malipo yao ya nauli na mizigo na fedha za kustaafu kupitia mifuko ya jamii. ningependa kujua hapa tatizo ni nini? Lipo pia tatizo la baadhi ya askari kukatwa madeni zikiwemo fedha za mikopo ya elimu ya juu, wakati mwingine askari hana elimu ya juu na wala hakuchukua mkopo. Swali, ningependa kujua hapa tatizo ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu posho ya chakula ya askari na posho ya vinywaji. Naipongeza Serikali kwa kuwapa posho ya chakula na posho ya vinywaji. Pia ningependa kujua posho ya nyumba kwa Askari wanaoishi uraiani kwa nini hazilipwi na lini zitalipwa? Ningependa kujua ni lini Serikali itawapa Askari Zimamoto posho ya nyumba na kuwajengea nyumba za kuishi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafunzo ya askari. Naipongeza Serikali kwa kuendelea kutoa mafunzo kwa askari wetu ili wawe na weledi na uelewa wa pamoja katika kutekeleza majukumu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua askari wanaokwenda kuchukua kozi mbalimbali za usalama barabarani, upelelezi na kozi nyingine gharama za mafunzo hayo nani analipa kwa sababu zipo taarifa kwamba, baadhi ya askari wanaokwenda kila askari atakatwa 7,000/= kwa siku, fedha ambayo hana uwezo wa kuilipa na pia, kuendesha familia yake. Ningependa kujua utaratibu huu umeanza lini na kwa nini Askari akatwe fedha yake ya chakula kwenda masomoni?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe na Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama na kutoa mchango katika hoja hii muhimu ya Makadirio ya Mapato na Matumishi ya Ofisi ya Rais, Utumishi kwa mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kuunga mkono hoja kwa sababu Serikali inafanya kazi nzuri ya utawala bora unaozingatia matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nampongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wengine kwa kazi nzuri wanayofanya na kwa kuandaa na kuwasilisha vizuri hotuba yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi, napenda kutoa ushauri katika maeneo machache yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kuhusu uhaba wa wafanyakazi. Pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Serikali ya kuajiri wafanyakazi katika sekta mbalimbali kama ilivyoelezwa kwenye hotuba ya Waziri bado tatizo la wafanyakazi ni kubwa sana na hasa katika sekta za afya, elimu na kadhalika. Nashauri Serikali iendelee kutafuta fedha kwa ajili ya kuajiri watumishi hasa katika sekta ya afya na elimu na hasa walimu wa sayansi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili niwatumishi wa kujitolea.Nashauri Serikali ianzishe mpango wa wafanyakazi wa kujitolea katika kada mbalimbali kama ilivyokuwa ikifanyika zamani. Hii ni kwa sababu wataalam tunazalisha wa kutosha na hawana ajira, hivyo, wakipata hata kazi ya kujitolea wataendelea kuongeza maarifa na uzoefu na kutoa mchango kwa taifa na nafasi zikipatikana wao ndiyo wapewe kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu ni kuhusu vibali vya kuajiri watumishi kupitia vyanzo vya ndani. Zipo taasisi ambazo zina uwezo wa kuajiri watumishi kupitia vyanzo vya ndani. Nashauri taasisi hizo zitambuliwe na kutoa nafasi za kuajiri watumishi kupitia vyanzo vya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika,nne ni upekuzi kwa viongozi na watumishi (vetting). Zoezi la upekuzi kwa watumishi wanaostahili kuongezewa madaraka lifanyike kwa wakati ili kupunguza tatizo la upekuzi kufanyika kwa muda mrefu na hivyo Halmashauri nyingi kukumbwa na tatizo la kuwa na watu wanaokaimu. Zoezi la upekuzi liendelee kufanyika kwa umakini na uadilifu ili kutotoa mwanya kwa watendaji na viongozi wasio waaminifu na waadilifu kupenya na kupewa nafasi katika vyombo mbalimbali vya maamuzi na umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nne ni mpango wa TASAF.Naungana na Kamati kuwa uhakiki wa kuondoa kaya zisizostahili ufanyike kwa umakini na uadilifu mkubwa ili wasiostahili waondolewe na wanaostahili wanufaike na mpango wa kuhudumia kaya masikini ikiwa ni pamoja na kuongeza wigo kwa kaya zingine zinazostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tano ni kuhusu TAKUKURU kudhibiti mali za umma. Napongeza TAKUKURU kwa kuendelea kufuatilia vitendo vya rushwa katika kutekeleza miradi ya maendeleo na katika taasisi za umma za kutoa huduma. Nashauri jitihada ziendelee ili kuokomesha vitendo vya rushwa na matumizi mabaya ya mali za umma ili nchi yetu iweze kufikia maendeleo tunayoyataka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha MUTEX Musoma kilichokuwa kinazalisha kanga na vitenge, kilitoa ajira 1,000, lakini tangu kibinafsishwe kiwanda hiki hakifanyi kazi hivyo kufifisha uchumi kwa Mkoa wa Mara na Taifa kwa ujumla. Kiwanda hiki kwa sasa kimekosesha ajira kwa Wanamara na hasa wanawake walikuwa wakifanya kazi kwenye kiwanda hiki. Je, ni lini kiwanda hiki kitarudishwa Serikalini au kutafuta muwekezaji mwingine?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia zipo taarifa kwamba mashine mpya zilizokuwepo katika kiwanda hiki kwa sasa hazipo tena na ziling’olewa. Je, Serikali wanazo taarifa za kiwanda hiki kuharibiwa miundombinu yake?

Mheshimiwa Naibu Spika, taulo za wanawake, watoto wa kike zinauzwa bei ghali hivyo wanawake na watoto wa kike wenye kipato cha chini kushindwa kumudu gharama na hata kuhudhuria masomo yao kikamilifu. Katika bajeti ya mwaka 2018/2019, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana alifuta kodi kwenye malighafi zilizotumika kutengenezea taulo za kike. Je, tangu tumeondoa kodi hizo ni viwanda vingapi vimejengwa hapa ndani kwa ajili ya kutengeneza taulo hizi? Kwa sasa bei imeshuka kwa kiasi gani ili kuleta unafuu kwa wanawake na wasichana?

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vya kutengeneza madawa hapa nchini; Tanzania tunatumia pesa nyingi katika kuagiza madawa kutoka nje ya nchi. Ningependa kujua ni viwanda vingapi vimejengwa mpaka kufikia sasa? Serikali ina mpango gani wa kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje ili kuwekeza hapa nchini badala ya kutegemea viwanda vya nje?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, nianze kukushukuru wewe na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uwezo wa kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu kuhusu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Naomba nianze kwa kuunga mkono hoja kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki cha 2019/2020 hali ya usalama wa raia na mali zao umeimarika. Pamoja na changamoto zilizojitokeza za mauaji ya watoto na kupotea kwa watoto katika Mikoa ya Njombe na changamoto za hapa na pale ambazo hazijakatisha tamaa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, kulinda raia na mali zao na wote tunaotambua na kuthamini kazi kubwa mnayoifanya, tunawatia moyo endeleeni kuchapa kazi. Watanzania walio wengi wanawaunga mkono na kuwaombea dua njema. Taarifa imeandaliwa na Mheshimiwa Waziri na timu yake, wanafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Spika, kuhusu bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani; pamoja na kuipongeza Serikali kwa kupeleka fedha kwa kiwango cha zaidi ya asilimia 86, nashauri fedha ya Wizara hii ipelekwe yote na bajeti iongezwe kwa sababu majukumu ya Wizara hii ni muhimu na nyeti kwa usalama wa raia, mali na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, maslahi ya Askari Polisi, Magereza, Zimamoto na Uhamiaji. Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Serikali yetu kuhakikisha inaboresha maslahi ya Askari wetu kwa kuwapa mishahara bila kukosa, kuwapa posho ya chakula, nyumba na kadhalika bado tatizo kubwa lililopo ni maslahi ya Askari wetu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri Serikali itazame upya mambo yafuatayo:-

(a) Mishahara ya Askari iongezwe;

(b) Posho ya chakula iongezwe na itolewe kila inapofika tarehe 15 ya kila mwezi kuliko inavyotolewa sasa mwisho wa mwezi;

(c) Posho ya nauli za likizo na safari za kikazi kwa Askari zilipwe kwa wakati kama inavyofanyika kwa watumishi wengine;

(d) Vitendea kazi kwa Askari wetu, mfano, uniform kwa sasa baadhi ya Askari wananunua wenyewe. Hili liangaliwe na zitengwe fedha za kutosha kwa ajili ya kununua nguo za Askari Polisi, Magereza, Uhamiaji na Zimamoto;

(e) Stahiki za Askari wanapostaafu zitolewe mapema ili kuondoa usumbufu kwa Askari wanaokaa muda mrefu bila kulipwa stahiki zao. Napendekeza taratibu za malipo na kila anachostahili Askari kupewa, kiandaliwe mapema kabla ya Askari kutoka kazini;

(f) Askari Polisi anapofiwa na ndugu wa karibu kama vile baba, mama, mke au mume, Askari hapati fedha ya rambirambi kama ilivyo kwa watumishi wengine; na

(g) Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa rambirambi kwa Askari anayefiwa na ndugu wa karibu kama ilivyo kwa wafanyakazi wengine.

Mheshimiwa Spika, makazi ya Askari Polisi, Magereza, Zimamoto na Uhamiaji. Pamoja na kuipongeze Serikali kwa ujenzi wa makazi na vituo vya Polisi na pia kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli mnamo tarehe 7 Aprili, 2018 wakati akizindua nyumba za Askari Mkoani Arusha, alitoa shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa makazi ya Askari ngazi ya chini ambayo fedha hiyo imesaidia kujenga nyumba 400 katika mikoa mbalimbali kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameeleza kwenye hotuba yake. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali, Serikali iandae mpango mkakati wa kujenga nyumba za Askari kwa kutumia rasilimali watu iliyopo katika Taasisi hizi kwa kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hizo. Serikali ifufue kitengo cha ujenzi kilichopo katika Jeshi la Polisi na Magereza na kuwatumia wataalam wa ujenzi waliosajiliwa na Bodi ya Wahandisi; licha ya uchache wao wangeweza kusaidia kuboresha hali ya majengo kupitia kikosi cha ujenzi cha Polisi au Shirika la Uzalishaji Mali la Polisi; lakini wafungwa wanapangiwa kazi za jumla vituoni (general duties) na Askari wenyewe.

Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali itoe fedha tuweze kujenga nyumba za Askari kama ilivyokuwa miaka ya nyuma. Askari Polisi na Magereza walijenga nyumba zao wenyewe kwa kutumia rasilimali fedha kidogo na rasilimali watu katika taasisi hizo. Swali, pia ningependa kujua kama Askari analipwa posho ya nyumba; na ni kwa asilimia ngapi?

Mheshimiwa Spika, pamoja na kupongeza utaratibu unaotumika wa kuwapandisha vyeo Askari Polisi, bado lipo tatizo la baadhi ya Askari kutopandishwa vyeo kwa wakati, jambo ambalo linaleta manung’uniko yasiyo ya lazima kwa baadhi ya Askari. PGO ya Jeshi la Polisi inaeleza, Askari atapandishwa Daraja/cheo kila baada ya miaka mitatu endapo Askari anatimiza masharti kwa mujibu wa PGO.

Napenda kujua ni kwa nini wapo Askari ambao wanatimiza masharti ya PGO mpaka sasa wamekaa muda mrefu bila kupandishwa vyeo na wengine wanakaa kwenye cheo kimoja miaka zaidi ya mitatu hadi miaka 10 na wengine mpaka wanastaafu?

Mheshimiwa Spika, pia masharti ya upandishaji wa vyeo yamekuwa yakibadilika tofauti na Uhamiaji na Magereza. Hapa napenda kujua, sababu ni nini?

Mheshimiwa Spika, Serikali imejenga blocks sita za makazi, ghorofa tatu zinazokaliwa na jumla ya familia za Askari 24 kutoka mikoa ya Mwanza, Bukoba na Musoma bado hazijakamilika toka mwaka 2010. Napenda kujua nyumba hizi zitakamilika lini ili Askari Polisi waweze kuishi humo na hasa kwa kuzingatia kuwa walibomolewa nyumba walizokuwa wakiishi? Pia Jeshi la Polisi lilikuwa na mpango wa kujenga mahanga katika kila Mkoa wa kuishi Askari wapya 96 katika baadhi ya Mikoa michache tu ila mahanga hayajajengwa. Napenda kujua je, mahanga yenye uwezo wa kubeba Askari wapya 96 kila Mkoa yatajengwa lini?

Mheshimiwa Spika, ningependa kujua je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ofisi za Polisi Mkoa na Wilaya ambazo hazijakamilika katika mikoa mbalimbali?

Mheshimiwa Spika, kuna vituo vya Polisi vimejengwa kwa nguvu za wananchi katika maeneo mbalimbali; mfano, Kituo cha mpakani mwa Malawi na Soko la Ileje na Kituo cha Malimbe Mwanzo: Je, Serikali ina mpango gani wa kuunga mkono nguvu za wananchi ili vituo hivyo viweze kukamilika na kutumika? Jeshi la Polisi lilianzisha mpango wa kujenga nyumba za Askari katika baadhi ya Mikoa na Ofisi za Mikoa na Wilaya. Napenda kujua mpango huu umekwamia wapi?

Mheshimiwa Spika, swali, nyumba za Askari Mkoa wa Mara hazijakamilika na kutumika, tatizo ni nini? Nyumba za Askari Mkoa wa Mwanza hazijakamilika, tatizo ni nini? Ofisi mbalimbali zimeanzishwa, zimeisha kwenye misingi tu kama Manyara na Mara.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kukushukuru wewe na Mwenyezi Mungu, Mungu muweza wa yote kwa kuniwezesha kusimama na kutoa mchango wangu katika sekta hii muhimu ya elimu, sayansi na teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono kwa sababu Waziri Profesa, Mama Ndalichako, Naibu Waziri Olenasha, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu, Dkt. Ave Maria, Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Wahadhiri, walimu na wafanyakazi mnaofanya kazi nzuri sana kwa bidii na maarifa, wavumilivu, waaminifu na kwa uadilifu mkubwa na pia taarifa imeandaliwa vizuri, ina data za kutosha zinatuonyesha wapi tulikotoka na wapi tulipo na wapi tunakwenda, ninawapongeza sana. Naomba tuendelee kuwatia moyo, niendelee kuwatia moyo, endeleeni kuchapakazi, tuna imani kubwa nanyi na Mungu atawabariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bajeti ya Wizara ya Elimu; Utekelezaji wa Fedha za Miradi ya Maendeleo ya Matumizi ya Kawaida; pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Serikali ya kupeleka fedha za mishahara, matumizi mengineyo ya fedha na miradi ya maendeleo kwa kiwango cha asilimia 60 ya Fungu Namba 46, naungana na uchambuzi wa Kamati kuwa lipo tatizo la upelekaji wa Fedha za miradi ya maendeleo ya fedha za matumizi ya kwaida.

Mfano, asilimia 37 kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya Wizara ya Fedha ambayo haikidhi kutekeleza kazi zilizopangwa na asilimia 62.8 haitoshi kutekeleza miradi ya maendeleo iliyopangwa na hivyo basi kusababisha kushindwa kulipa fedha za nyumba za Wahadhiri, kukamilisha miradi ya maendeleo kama ilivyokusudiwa. Mfano, Chuo Kikuu Kishiriki cha DUCE na Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kama ambavyo taarifa ya Kamati imeeleza. Ushauri:-

(a) Upelekaji wa fedha; naomba niungane na maoni yaliyotolewa na Kamati kuwa fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya sekta hii zipelekwe zote kama zilivyopitishwa na Bunge kabla ya mwaka wa fedha haujamalizika.

(b) Kubuni vyanzo vya mapato; pia nichukue nafasi kushauri Taasisi za Wizara hizi kuendelea kubuni vyanzo vya ndani ili kutekeleza miradi ya maendeleo na shughuli za uendeshaji kama ilivyofanyika katika vyuo vya DUCE na Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kama ambavyo Wajumbe wa Kamati tulijionea na leo taarifa imewasilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chuo Kikuu cha Mwalimu Julius K. Nyerere cha Sayansi ya Kilimo na Tekonolijia; ilani ya CCM, ukurasa wa …. Ibara ya 52, Kifungu cha (k)(2) imetamka bayana kuwa katika kipindi cha 2015-2020, Serikali ya CCM itakamilisha ujenzi wa Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi Shirikishi cha Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Butiama) lengo ikiwa ni kuenzi wazo la Baba wa Taifa ambaye yeye siyo kutoa wazo yeye na Ndugu zake, Watima walitoa eneo tena bure wakaanza kujenga miundombinu ya maji, Bwawa la Kialano n.k.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupongeza Serikali kwa kazi zinazoendelea kama ambavyo Waziri ameeleza kwenye ukurasa wa 85 wa hotuba yake.

Mheshimiwa Mwenyakiti, maswali - Hati ya Kiwanja; hati ya kiwanja inapatikana lini? Na kiasi cha fedha kilitengwa na ujenzi unaanza lini? Naomba Waziri utakapokuwa unajibu tusaidie kujua ili wananchi wa Wilaya ya Butiama (Mara) na Watanzania kwa ujumla wasikie kwa sababu lengo la CCM la kuanzisha Chuo hiki siyo tu ni kwa ajili ya kumuenzi Mwalimu pia ni kuongeza wataalam katika sekta ya Kilimo na teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu bila malipo; napenda kuchukua nafasi hii kwa niaba ya wanawake ninaowaalika kuleta shukurani nyingi kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa fedha za zaidi ya kiasi cha milioni 23 kwa ajili ya kugharamia elimu na kuwezesha watoto wa familia za wanawake na watanzania wanyonge, watoto hao kupata fursa ya kusoma bila vikwazo. Pamoja na pongezi hizo, naomba kushauri yafuatayo:-

(a) Mpango endelevu wa elimu bila malipo - Serikali tubuni chanzo cha mapato cha uhakika cha kutekeleza mpango huu kama ilivyo kwenye umeme vijiji na kwenye barabara.

(b) Ujenzi wa miundombinu; Serikali ishirikiane na wananchi kujenga miundombinu kama vile madarasa, mabweni, nyumba za walimu, vifaa vya kufundishia na vya kujifunzia, kuendelea kuongeza walimu hasa walimu wa masomo ya sayansi, upatikanaji wa madawati n.k kwa sababu kwa sasa kuna baadhi ya shule darasa moja na wanafunzi 60 mpaka 200.

(c) Vyuo vya VETA; naipongeza Serikali kwa kuendelea kujenga vyuo vya VETA katika Mikoa na Wilaya mbalimbali hapa nchini. Nashauri tuendelee kuongeza miundombinu ya vyuo vya VETA ili viwe na uwezo wa kuwapokea vijana wengi zaidi kuliko ilivyo sasa.

(d) Serikali iendelee kukamilisha ujenzi wa vyuo vya VETA katika Wilaya zote hapa nchini na kuanzia tuanze na wilaya zenye miundombinu ya majengo, vilivyokuwa vyuo vya wananchi kama vile Wilaya ya Bunda, Kisangwa, Chuo cha Wananchi-Bweri, Musoma Mjini n.k.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utoro shuleni na mimba za utotoni; pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Bunge kutunga Sheria kali kwa wale wote watakaomzuia mtoto kusoma kwa namna yoyote, hili tatizo la utoro limeendelea kuwa kubwa sana pamoja na mimba za utotoni. Ili kupunguza utoro shuleni, suala la chakula kwa watoto liwekewe mpango maalum unaotekelezaka. Ushauri wangu kwa Serikali, naomba suala hili la utoro mashuleni Serikali na jamii tulivalie njuga kwa kutumia Sheria hiyo tukakomesha utoro na mimba shuleni kwa sababu upo ulegevu wa utekelezaji wa Sheria hiyo kwa kisingizo hakuna ushahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi ya Bodi ya Mikopo; naomba kumshukuru Rais wetu kipenzi cha Watanzania kwa kutambua changamoto ya fedha za mikopo na kufanya suaa la kutoa fedha za mikopo kuwa ni mambo ya vipaumbele katika mipango ya Serikali ya kugawa rasilimali ya Taifa. Jambo ambalo limewezesha sasa Bodi ya mikopo kutoa mikopo kwa vijana wetu 1,227,583 mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 424,758,636,617.00, kukusanya madeni ya shilingi 128,076,510,388.48 sawa na asilimia 81.2, kati ya fedha 1577 zilizokuwa zinadaiwa. Pongezi nyingi sana. Pamoja na pongezi naomba kushauri yafuatayo:-

(a) Naomba Serikali iwe na mipango mizuri hata ya kujidhamini katika Mabenki kupitia mtaji tulionao ambao Serikali imekwishautoa ili suala la mkopo liwe kwa vijana na watoto wetu wote wenye uhitaji.

(b) Utaratibu wa elimu za ujazaji fomu ya maombi ya mikopo itolewe kwa watoto wote waliopo kwenye shule za sekondari na elimu kupitia mitandao mbalimbali ili kutoa fursa kwa vijana na wazi kuwa na uelewa wa pamoja juu ya vigezo vya kupata mikopo na utaratibu wa kujaza fomu na kuzifikisha katika Taasisi kwa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa miundombinu katika vyuo vikuu; pamoja na kazi nzuri inayofanyika ya kujenga miundombinu katika vyuo vyetu hapa nchini. Ningependa kujua Je, Serikali imejipangaje kujenga Mabweni katika vyuo vya ufundi vya Vyuo Vikuu ili kuondokana na changamoto inayokabili vijana wetu hasa wasichana kushindwa kulipa kodi katika nyumba wanazopanga, kutembea umbali mrefu n.k. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga miundombinu, barabara na majengo yenye hadhi ya jina la Chuo – Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa SADC na kuendesha vyema Mkutano wa 39 wa Jumuiya hiyo
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nami kwa niaba ya wanawake wenzangu walioko ndani ya ukumbi huu na wanawake wa Tanzania ambao sisi Wabunge wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tunawawakilisha, napenda kuunga mkono azimio hili lililowasilishwa asubuhi ya leo kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya kwanza naunga mkono azimio hili la kumpongeza Rais kwa sababu Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alikubali kwa niaba ya Watanzania kwamba Mkutano huo wa SADC ufanyike nchini Tanzania ambako ni heshima ya Watanzania wote na ikiwa ni ishara tosha ya kumuenzi baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na hayati Mzee Karume.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono azimio hili kwa sababu ni ukweli usiopingika Mkutano wa SADC uliandaliwa vizuri chini ya uongozi wa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kweli mkutano huu ulitupa hadhi na heshima Watanzania kuendelea kuwa champion wa ukombozi wa Bara la Afrika ikiwemo nchi za SADC. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono, azimio hili la kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu amepokea kijiti hiki cha kuwa Mwenyekiti wa SADC kutoka kwa Rais wa Namibia ikiwa nchi ya Tanzania na nchi za SADC tukiwa na amani na usalama. Ninapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono azimio hili la kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na si mwingine ni kipenzi chetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, aliongoza vema Mkutano wa SADC haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono kwa sababu kupitia Mkutano wa SADC Rais wetu kipenzi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alishawishi Marais wenzake na wakakubali lugha ya Kiswahili, lugha ambayo ni tunu ya Tanzania iwe sasa ni lugha ya nne katika nchi za SADC. Haijapata kutokea na katika hili hatutakaa tumsahau Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa kuleta azimio hili tumpongeze Mheshimiwa Rais, kwa kweli tunampongeza na tunakushukuru sana. Naunga mkono azmio hili la kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu ameendelea kushawishi Marais wenzake na nchi za SADC ziendelee kujitegemea kiuchumi kwa kutumia rasilimali zake ili nchi za SADC ziondokane na utegemezi; na akanukuu akasema, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na pale alipopumzika alisema kujitawala ni kujitegemea na mtaji wa masikini ni nguvu zake mwenyewe; na uwezi kuwa uhuru kama nchi yako haijitegemei. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuendelea kusisitiza nchi za SADC kujitegemea na yeye mwenyewe akawa ndiyo mfano wa kuifanya Tanzania sasa ijitegemee na mfano hata wa bajeti hii, tulikuwa ni tegemezi kwa asilimia 40. Sasa Tanzania tunajitegemea kwa asilimia nane. Hiyo peke yake tuna kila sababu ya kutaka kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Naunga mkono azimio hili, hongera sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Wanawake wa Tanzania tunakupongeza tuko pamoja na wewe. Ninachokuhakikishia, uchaguzi wa 2020 kura zote ni zako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono azimio hili. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe na kumshukuru Mwenyezi Mungu aliye juu Mbinguni kwa kunipa nafasi ya kusimama na kuweza kuchangia hoja hii muhimu ya Sekta ya Huduma za Jamii na Masuala ya UKIMWI ambayo mimi Amina Nassoro Makilagi ni Mjumbe wa Kamati zote hizi mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya shukrani, naomba nianze kwa kuleta salamu za wanawake na wananchi wa Tanzania walionipigia kura za kishindo wakanileta hapa Bungeni. Wamenituma nije niseme yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, wanamshukuru Mheshimiwa Rais na Serikali yake ya Chama cha Mapinduzi kwa kuboresha huduma za afya, kwa kutenga fedha za kutosha za kuhakikisha tunapata dawa, vifaa tiba na vilevile tunaboresha miundombinu. Wenzangu wameshasema, sitataka kurudia; na kama alivyosema Mbunge wa Mkoa wa Mara, Mheshimiwa Vedastus Mathayo, kwa miaka hii ya hivi karibuni tunashuhudia Hospitali za Rufaa zaidi ya 10 zinajengwa katika nchi hii. Mkoa wa Mara peke yake tumepata zaidi ya shilingi bilioni
15. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nianzie hapo kuleta salamu za wananchi wa Simiyu, wanashukuru sana kwa Hospitali ya Rufaa na pia ninaleta salamu za wananchi wa Geita, wanashukuru sana na ninaleta salamu za wananchi wa Katavi, wanashukuru sana, wananchi wa Songwe na wananchi wa Geita na Mkoa wa Mara wanashukuru sana na hata Mkoa wa Mtwara. Wanaomba Serikali iendelee kuleta fedha za kutosha ili Hospitali za Rufaa ziweze kukamilika, hasa kwa kuzingatia kwamba Kanda ya Ziwa mfano Hospitali ya Rufaa ya Bugando imezidiwa, Hospitali ya Mwalimu Nyerere Memorial Centre itasaidia kukabiliana na ile changamoto ya watu (population) ya zaidi 15,000 ambao wanahudumiwa katika Hospitali ya Bugando.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata ule Ukanda wa Mtwara hapakuwa na Hospitali ya Rufaa, kwa hiyo, wamekuwa wakipata adha ya kuja Muhimbili. Nina imani sasa changamoto inaenda kutatuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali na wanawake wa Tanzania wamenituma nije kuleta ahsante kwa kujenga hospitali 67. Wanawake wanasema ahsante sana, Mungu amjalie Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, aendelee kutenga fedha kwa zile Halmashauri ambazo hazijafikia mpango huu kwa mwaka wa fedha ujao 2020/2021, nao waweze kupata fedha na hospitali zijengwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala zima la kupunguza vifo vya wanawake na watoto; wanawake wamenituma, wanasema wanaishukuru sana Serikali ya CCM kwa kujenga vituo zaidi ya 350 jambo ambalo limepunguza kasi ya vifo vya wanawake na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninayezungumza, nimetembea ziara kabla ya kuja hapa, kwenye Mkoa wa Mara nimetembelea vituo vyote na mikoa ya jirani nimekwenda, kwa kweli hali ni nzuri, tunashukuru sana na wanawake wamenituma nije niseme ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ushauri ninaoutoa kwa Mheshimiwa Spika, tumefanya kazi nzuri ya kujenga vituo, tumefanya vizuri kuboresha huduma, lakini naungana na wachangiaji wenzangu kwamba Serikali itafute fedha kwa ajili ya kuajiri wataalam. Maana tusipoangalia, tumejenga vituo, lakini havifanyi kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niwashauri pia kwamba ni vizuri Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na TAMISEMI, wafanye hizo tathmini kuona tangu tumejenga hivi Vituo vya Afya ni vingapi vinafanya kazi? Kwa sababu, mfano nimetembelea Kituo cha Kinesi, Kituo kimeshajengwa, kimekamilika lakini pale hakuna Mtaalam wa Usingizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetembelea Kituo cha Nata Isenye Serengeti Kituo kiko vizuri na huduma zimetolewa lakini yupo daktari mmoja; nimekwenda kule Butiama hakuna mtaalamu wa mionzi lakini pia hakuna x-ray. Kwa kweli tunaweza tukajenga baadaye tukabaki na Majengo nilikuwa naomba sasa Mheshimiwa Waziri na timu yake hebu sasa tujielekeze kwenye wataalamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hapa ushauri ninaoutoa kama alivyosema Mheshimiwa Tendega ambaye ni mjumbe mwenzangu wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii tumekuwa tukitoa ushauri chini ya Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Peter Serukamba; kwamba sasa ifike wakati Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto iwatambue wataalamu wa sekta ya afya iongee nao, izungumze nao iwaombe wajitolee. Sisi wenzenu tulianza kujitolea; hata mimi hapa nilipo sikufika hapa leo nikawa Mbunge, sikufika hapa nikawa Katibu Mkuu, nilianza kujitolea. Mimi nilijitolea miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wataalamu ambao wako tayari wanasubiri ajira, wapo wataalamu ambao wanasubiri kupewa ajira Serikalini ni vizuri tukazungumza nao halafu kupitia vyanzo vya ndani wakalipwa fedha kidogo kwa ajili ya kujikimu ili waweze kutoa mchango wao katika taifa. Vilevile kuna watu waliostaafu kazi, wako huko wamestaafu na bado wana nguvu kabisa; miaka 60, miaka 55, ni wataalamu wetu wanaweza wakashirikishwa ili waweze kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoshauri tena katika mwaka wa fedha ujao 2020/2021 tuje na bajeti nzuri itakayotoa fursa kwa Serikali kuweza kuajiri Wataalamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa elimu naleta shukrani nyingi sana kwa wananchi na wanawake wa Tanzania kwa kazi nzuri sana inayoendelea ya kuhakikisha vijana wetu waliopata fursa ya kupata elimu ya juu wanapata mikopo. Ni ukweli usiopingika kwanza kwa kipindi hiki kifupi zaidi ya shilingi bilioni mia nne zimeweza kutoka kwaajili ya vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, kwenye sekta hii ya kutoa mikopo kwa elimu ya juu hebu tufanye uwiano ulio sawa kwa upande wa vijana wa kike ili na nao waende sambasamba kwa sababu takwimu zinaonesha kwamba watoto wa kike wamebaki nyuma kidogo. Vilevile nataka nitoe tena ushauri kwenye kupeleka watoto wa elimu ya juu katika vyuo vikuu; hata ukiangalia takwimu pia uwiano hauendi kati ya wanawake na wanaume bado wanawake wako chini. Nilikuwa nashauri hebu tupandishe hii na wanawake wapate hii fursa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niache salamu za wananchi; wanashukuru sana jinsi ambavyo Serikali imeendelea kutoka mikopo. Ni hivi karibuni tu kupitia takwimu tulizozipata kupitia huduma za jamii ni zaidi ya shilingi milioni mia nne na themanini zimetolewa kwa ajili ya mikopo. Tumetoka mbali kazi ni nzuri tunaomba fedha ziendelee kutengwa ili akina mama vijana wetu waendelee kupata mkopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa elimu ya dekondari tumefanya kazi nzuri, vijana wetu sasa wanakwenda wengi, na hata kwenye shule za awali wanakwenda, wenzangu wamezungumza, nisirudie. Hata hivyo hapa ushauri wangu, tujitahidi sasa kwenye walimu wa sayansi. Kusema ukweli kuna changamoto ya sayansi katika elimu ya sekondari na msingi. Kama nilivyoshauri kwenye sekta ya afya, tutafute fedha ili tuwapate na walimu wa sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la. Kadri tunavyoongeza watoto; majengo ni yale yale; na bahati nzuri wananchi wanafanya kazi nzuri ya kujenga maboma. Nitatolea Mkoa wa Mara ninakotoka; sisi Mkoa wa Mara hatusubiri Serikali ijenge kuanzia msingi, sisi tunajenga mpaka renta. Wananchi wanahitaji haya maboma sasa yatengewe fedha kwa ajili ya kukamilika. Tunashukuru sana Serikali kwa kutuletea fedha shilingi bilioni mbili kwa ajili ya Chuo cha VETA.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mungu awabariki, naunga Mkono hoja. (Makofi)