Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Anatropia Lwehikila Theonest (67 total)

changamoto kubwa ya zahanati hizi katika Jimbo la Segerea na Manispaa ya Ilala ni maeneo lakini wapo watu wanaoishi jirani na maeneo hayo, wapo tayari kutoa maeneo yao kwa ajili upanuzi wa maeneo ya zahanati hizi.
Je, Serikali ipo tayari kusaidiana na Halmashauri ya Ilala kulipa fidia kwa ajili ya kuongeza ukubwa wa maeneo ili kupata zahanati na vituo vikubwa vya afya katika maeneo ya Jimbo la Segerea na Manispaa ya Ilala kwa ujumla?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kama nilivyosema katika jibu letu la awali, mahitaji ya afya hapa yamekuwa ni changamoto kubwa sana, nilipofanya reference tulipokuwa na Mbunge wa Segerea kipindi kilichopita, alipokuwa na timu iliyoenda eneo la Vingunguti katika machinjio yale, vilevile akaja katika ofisi yangu kuona jinsi gani tutafanya, licha ya suala la machinjio lakini wananchi wana changamoto ya afya.
Mheshimiwa Spika, mimi naamini hayo mawazo ni mazuri, tutakaa vizuri kubadilishana mawazo ili tuone ni jinsi gani tutafanya ujenzi wa zahanati au kituo cha afya maeneo yaweze kupatikana. Lengo kubwa ni kwamba kina mama na watoto wa maeneo yale waweze kupata huduma kama wengine.
Mheshimiwa Spika, ajenda yetu kubwa ni kuhakikisha kwamba hospitali zetu za rufaa sasa tupunguze idadi ya wagonjwa siyo mtu anaumwa mguu mpaka aende Muhimibili au Amana haiwezekani hata kidogo. Lazima tuhakikishe mfumo mzuri unatengenezwa katika sekta ya afya katika ngazi za chini kusaidia sekta za juu ziweze kufanya huduma kubwa zinazohitajika.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Spika, swali la Kigoma Kaskazini linafanana kabisa na swali la wananchi wa Segerea na Ukonga. Wananchi wa Kipunguni A, Kipunguni Mashariki, Kipawa na Kigilagila waliambiwa wapishe maeneo yao kwa ajili ya ujenzi au upanuzi wa uwanja wa ndege. Wanachi hawa wamefanyiwa tathmini tangu mwaka 2007, imekuwa ni danadana, sasa Waziri atuambie ni lini wannachi hawa watalipwa fidia baada ya kuwa wanapewa pesa kidogo wanaambiwa watalipwa na siku zinakwenda na wanashindwa kuendeleza maeneo yao.
Je, ni lini, fidia hizo zitalipwa na hawa wananchi waweze kupata maeneo mengine ya kujisitiri? Wananchi hao wanamsikia. Nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, Mbunge wa Segerea anafahamu kwamba tulikaa kikao…

Naomba nipewe fursa ya kujibu swali.
Mheshimiwa Mbunge wa Segerea alishafanya kikao na mimi mwenyewe kuniita, katika kikao hicho nilikutana na wahusika wote wanaotakiwa kulipwa fidia katika eneo la Kipunguni. Kwa hiyo, namshukuru sana, kwanza Mheshimiwa Anatropia kwa kumuunga mkono Mbunge mhusika katika eneo hili na Mbunge mhusika katika eneo hili anafahamu kwamba nimeshatoa ahadi ya kuhakikisha suala la kulipa fidia eneo la Kipunguni kwa ajili ya kupisha ujenzi wa uwanja wa ndege nitalishughulikia na litafikia mwisho katika kipindi hiki cha miaka mitano na anafahamu sababu yake.
Mheshimiwa Spika, sababu yake ni kwamba kuna fedha ilishatolewa, lakini kuna uwezekano fedha zilizotolewa zote hazikuwafikia walengwa. Kwa hiyo, tumeunda Tume inafanya uchunguzi wa suala hili kuhakikisha zile fedha zilizotakiwa kuwafikia walengwa tujue zimeenda wapi na tutafunua kila palipofunikwa kuhakikisha fedha zile zilizokusudia kulipa wahanga wale zinapatikana na hatimaye wahanga walipwe. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilimhakikishia Mbunge mhusika wa hilo eneo na sasa naomba nimhakikishie Mheshimiwa Anatropia, suala hili tumelichukua kwa nguvu na tutalishughulikia, tutafukua kila aina ya kaburi kuhakikisha kwamba wahusika wanalipwa fidia iliyostahili. Nilitoa katika mkutano ule wa wadau kwamba ni katika kipindi hiki cha miaka mitano.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika siku za hivi karibuni tumeshuhudia leseni za kufanya biashara katika Manisapa mbalimbali zinatolewa baada ya kupatikana kwa tax clearance, lakini ukweli ni kwamba sio biashara zote hasa biashara ndogo zinahitaji wakati mwingine tax clearance, haioni ni wakati muafaka kuweka categories za biashara ambazo wanaweza kupewa leseni bila hata tax clearance badala ya kinachofanyika sasa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hili ni swali la kutoa leseni ambalo ni swali jipya ambalo tumeondoka katika riba, kwa hiyo naomba niseme tu tuna viwango ili kuweza kutoa leseni katika biashara zote zinazoendeshwa ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, kama hawajafikia ndani ya kiwango kile kinachohitajika mfanyabiashara huyo wala hatozwi na wala hapewi leseni lakini akishavuka yale malengo ya biashara yake tayari anatakiwa apewe leseni na tunasimamia kama moja ya njia za kukusanya mapato yetu.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa taarifa zinaeleza kwamba, vyeti vimekuwa vikizalishwa nje ya nchi. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzalisha vyeti hapa nchini ili zoezi la kuvitoa liwe rahisi zaidi? Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa nilizonazo mimi vyeti vinatengenezwa hapa hapa nchini, tuna vifaa vya kisasa, Baraza la Mitihani lina vifaa vya kisasa sana na ni taasisi ambayo kwa ufanisi wake nchi nyingi sasa hivi zimeanza kuja kujifunza namna tunavyofanya. Kama Mbunge ana taarifa tofauti na hizi naomba tuonane baada ya Bunge hili ili nijue kwa nini yeye ana taarifa ambazo si sahihi.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo changamoto kubwa sana ya barabara kutokana na mitandao ya maji na hasa katika kata mbalimbali za Jimbo la Segerea ikiwemo Kata ya Vingunguti; je, ni kutokana na ubovu wa mabomba ndiyo maana tunazidi kuona maji yanazidi kutiririka hovyo katika maeneo haya?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, changamoto hiyo ipo. Kama tunavyokumbuka, wakati nilipotembelea barabara ya Kwa Mnyamani kutoka hapa Buguruni barabara ya Kwa Mnyamani kwenda Vingunguti, barabara ile muda mwingi sana maji yamejaa barabarani’ Tatizo kubwa ni kwamba yale mabomba yanapasuka kwa hiyo yanajaa barabarani na barabara inaharibika.
Mheshimiwa Naibu Spika, na ndiyo maana nilitoa agizo pale kwamba Manispaa yetu ya Ilala, TARURA pamoja na DAWASCO waweze kukaa pamoja kuangalia ile miundombinu yote ambayo iko barabarani iwekwe vizuri. Bahati nzuri zoezi hilo limekamilika, hivi sasa linaendelea vizuri, niwashukuru sana DAWASCO, pia niwashukuru Manispaa ya Ilala kwa kazi kubwa waliyofanya, na hivi sasa hata ile barabara tunaiboresha, sasa itakuwa kwa kiwango cha lami yote kuanzia hapa Buguruni tunapoingilia mpaka unafika Vingunguti.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili limefanyika shirikishi, kwamba maeneo hayo sasa yawe yanapitika vizuri, vilevile na mitandao ile ya maji ambayo inachanganyana sana wataalam nimewaagiza waiweke vizuri kuhakikisha kwamba tunalinda barabara zetu hizi. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Majibu ya Naibu Waziri tumeyasikia wakati wote. Mradi wa mfereji anaousema wa DMDP ni mradi ambao tumeambiwa utatekelezwa tangu mwaka 2014 na wakazi wa kata zinazopitiwa na mradi huo waliambiwa wasiendeleze maeneo yao tangu 2014 wakiendelea kuhangaika na mafuriko kila siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna changamoto ya madaraja na barabara Kata ya Bonyokwa, Kata ya Kinyerezi, Kata ya Segerea, Kata ya Liwiti na kubwa kuliko ni Kata ya Tabata katika barabara ya kwenda Mwananchi, kalvati limebomoka na kwa sasa ninavyoongea…

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali; je, ni lini mradi huo mkubwa wa DMDP utajengwa na barabara au Daraja la Kisiwani? Swali la kwanza.
Swali la pili, uanzishwaji wa TARURA umeondoa uwajibikaji wa Halmashauri sambamba na Madiwani moja kwa moja katika ujenzi wa barabara za mitaa. Je, Wizara ina mkakati gani kuhuisha kazi za TARURA ili waweze kutoa report katika Baraza la Madiwani ambalo moja kwa moja ndiyo wanawajibika kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kujua kero zao za moja kwa moja za barabara? (Makofi). Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Theonest amesema imekuwa ni muda mrefu hadithi imekuwa ikisemwa, lakini utakubaliana nami kwamba katika majibu yangu kwenye swali la msingi, nimemwambia kwamba kandarasi tunatarajia itatangazwa mwezi Mei na mwezi Mei siyo mbali sana, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, tumeahidi tutatekeleza katika hili ambalo nimelisema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameongelea juu ya suala zima la uanzishwaji wa chombo hiki cha TARURA na anachoomba ni namna gani TARURA watahuisha ili wananchi waweze kupata ushiriki wao kwa kupitia Waheshimiwa Madiwani na Wabunge?
Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA ina wajibu wa kuhakikisha kwamba taarifa zake zinapelekwa DCC na DCC Waheshimiwa Wabunge ni Wajumbe, lakini Mwenyekiti au Meya ni Wajumbe na Wakurugenzi ni Wajumbe. Kwa hiyo, taarifa itakuwa inatolewa hapo na tutapata fursa ya kuweza kuwahoji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, pia kwenye chombo cha RCC ambapo sisi Waheshimiwa wote ni Wajumbe, naomba tushiriki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijaribu kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge kwamba kabla ya kuanzishwa kwa TARURA kila Mbunge na hasa kila Diwani alikuwa anaomba apate angalau hata kilomita moja ya kipande cha barabara au kalavati litengenezwe upande wake kiasi kwamba ule ufanisi (value for money) ilikuwa haionekani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tukienzi chombo hiki, bado ni mapema kabisa. Maeneo mengine ambayo TARURA imeanza kufanya kazi, wanapongeza. Naomba tukiunge mkono. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nadhani waliomwandikia Mheshimiwa Naibu Waziri hawakunielewa vizuri. Swali langu nimeuliza hivi, ni kwa kiwango gani barabara za mitaa ina maana kutoka barabara ya Segerea kwenda Mandela road tutaweza kupunguza foleni. Kwa maana tutafungua vipi barabara za mtaa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wameainisha kwamba wametenga fedha ya ujenzi wa barabara kutoka Barakuda
- Chang’ombe, sasa ukitoka Barakuda - Chang’ombe bado hawajapunguza foleni. Wangesema kutoka Barakuda - Chang’ombe - Kimanga ili wananchi wapite Kisiwani wasiingie Mandela road. Vivyo hivyo kutoka Kinyerezi - Kimara watu waingie Morogoro road wasirudi barabara ya Segerea, tuna changamoto sana ya foleni. Vivyo hivyo …
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali ni lini barabara ya Segerea itapunguziwa foleni kwa kuboresha barabara za mitaa zinazotoka na siyo kurudi barabara kwenye moja? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wamesema wametenga fedha kwa ujenzi wa daraja wa Tabata Kisiwani. Namwomba Naibu Waziri aje tumuonyesha daraja hilo kwa sababu lina changamoto kubwa. Matajiri wamevamia eneo, daraja haliwezekani kwa sababu mkondo ni mdogo. Ni lini atakuja kuona changamoto ili kuwaondoa wale watu tuweze kujenga daraja pale? Vinginevyo ni kupoteza fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu la msingi nimeeleza barabara ambazo zinatengenezwa na tafsiri yake ni nini? Mwananchi ambaye alikuwa anataka kwenda Segerea ana-option ya kutumia barabara ya zingine na ambacho kimekuwa kikitokea ni kwamba hizi barabara zikiwa mbovu sana hata ambaye angeweza kupita kwa Mnyamani hawezi kupita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kadri barabara hizi zingine zinavyotengenezwa inampa nafuu mwananchi wa maeneo hayo. Si kwamba gari zote ambazo zinazopita huko wanataka ni kwa sababu barabara za mtaani zinakuwa siyo nzuri. Aidha, kwa Jiji la Dar es Salaam kuna mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba tunali-decongest, mpango uko vizuri, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira hilo liko mbioni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusiana na daraja ambalo analizungumzia na kuuliza nitakwenda lini, weekend iliyopita nilienda nikafika mpaka Mnyamani bahati mbaya tu Mheshimiwa Mbunge hakuwa na taarifa. Mimi niko tayari kwenda kwa kadri nafasi itakavyoruhusu ili tukatizame site kuona nini kilichopo ili tuweze kushauri vile ambavyo inatakiwa.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niweke rekodi sahihi; swali langu halijajibiwa, nimeuliza kilometa tano za lami zilizoahidiwa na Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni katika Kata ya Kyerwa. Hii ni kata ya mjini, ina wafanyabiashara wengi, ina shughuli nyingi za kibiashara lakini watu wanateseka na adha ya vumbi inayosababisha ajali mbalimbali za mabasi, boda boda na magari mengine.
Swali ni lini kilometa tano alizoahidi Mheshimiwa Rais katika Kata ya Nkwenda – kata ya kibiashara – zitajengwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; tumeshuhudia taharuki na bomoa bomoa katika Kata hii ya Nkwenda ambayo hatuoni kama imetengewa bajeti lakini bomoa bomoa na X zinaendelea. Swali, wale wanaowekewa X na kubomolewa nyumba zao watapewa fidia kwa kuwa hakukuwa na ramani ya mpangomji na ramani sasa inawafuata watu wakiwepo pale; watapewa fidia katika maeneo yao ambayo yanakwenda kupitiwa na bomoa bomoa ya ujenzi wa barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika majibu yangu ya msingi, unapoanza kujenga kilometa tano ukaanza na kilometa moja tayari ulishaanza ujenzi kuelekea kilometa tano ambazo Mheshimiwa Rais ilikuwa ahadi yake. Kwa hiyo, nimemhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi ya Mheshimiwa Rais ambayo wajibu wake ni kutekelezwa ndani ya miaka mitano na kuhakikisha kwamba ahadi hizo zinatekelezwa ndiyo maana tunaanza na kilometa moja. Ukijenga kilometa moja katika tano zinakuwa zimebaki kilometa nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia anauliza juu ya wananchi kulipwa fidia. Sheria iko wazi, kwa wale wananchi ambao wameifuata barabara ambayo; hatuwezi wakati huo huo tukataka maendeleo na wakati huo huo tukataka tubaki katika hali ile kabla ya maendeleo. Kwa hiyo, kwa wale ambao wameifuata barabara hawatalipwa na wale ambao barabara imewafuata watalipwa kwa mujibu wa sheria.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa ukataji wa leseni unaenda sambamba na uwasilishaji wa tax clearence katika Halmashauri zetu na uwasilishaji wa tax clearance unaamaanisha kwamba watu wamelipa kodi, kwa maana hiyo watu wanalazimika kulipa kodi kabla hata ya kufanya biashara. Je, hatuoni kwamba ni muhimu kuondoa kigezo cha tax clearance katika baadhi ya biashara ili watu waweze kukata leseni na kuanza biashara kabla ya kulipa kodi na kabla ya biashara zenyewe kuanza? (Makofi) Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake linalenga kujaribu kutetea wafanyabiashara wale wanaoanza na utetezi wa aina hiyo siyo mbaya, ni mzuri. Hata hivyo, kwa sababu kuna kanuni, sheria na taratibu ambazo zimewekwa, nalichukulia swali lake kama mchango wa maoni ambao unahitaji kufanyiwa kazi baadaye lakini kwa leo hatuwezi kutoa tamko kwamba sasa tunafuta taratibu hizo. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru swali la nyongeza la kwanza, ni ukweli kwamba idadi ya akinamama wanaoendelea kujifungua kulingana na takwimu inaendelea kuongezeka, lile jengo kusema ukweli bado ni finyu sana kiasi cha kupelekea akinababa kushindwa kuandama na wenza wao, kinyume na alivyosema Naibu Waziri. Sasa swali langu sio kweli kwamba jengo lile haliwezi kubadilishwa, jengo linaweza likaondolewa likajengwa ghorofa angalau moja au likajengwa ghorofa moja sehemu nyingine Serikali ipo tayari kutenga bajeti kwa ajili ya kujenga eneo angalau la ghorofa moja kuweza kuwa-accommodate watu hawa ambao wanabanana kwenye corridor?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kujifungua ni tendo la faragha sana, wote mtajua Madaktari akinamama wanavyoenda kwenye hicho kitendo wengine wanaweza kutoka vinyesi, wengine wanapata kifafa cha mimba, wengine wanatokwa na maneno ya ajabu na shida nyingine kama hizo ambao wamepitia uzazi wanajua, ni kwa nini Serikali haioni umuhimu wa kutengeneza vyumba ambavyo concrete au ku-separate vile vitanda na concrete au kujenga partition ambazo mwanamke mmoja na mwingine hawawezi kuonana tofauti na ilivyo leo kwamba mmeweka pazia ambazo kiukweli wanaonana na inadhalilisha utu wao. Naomba sasa Serikali ituambie ni lini ipo tayari kutengeneza partition kwa ajili ya kustiri utu wa mwanamke pale anapokwenda kujifungua.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSI NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia. Kwanza suala kwa nini tusiongeze jengo lingine Muhimbili Mheshimiwa Mbunge alitakiwa kutushukuru kwa sababu lile ni jengo la ziada, baada ya Mheshimiwa Rais mara tu baada ya kuapishwa alikuta mrundikano wa wangojwa akatunyang’anya ofisi Wizara ya Afya na jengo lile tukaliboresha na kuwa ni jengo la Wazazi.

Mheshimiwa Spika, nashukuru umenipa fursa ya kujibu hili swali. Muhimbili National Hospital, tumefuta kliniki za mama na mtoto katika Hospitali za Rufaa za Mikoa na Muhimbili. Pale tunapeleka wajawazito ambao wana matatizo ya kujifungua. Kwa hiyo hata ule mrundikano wa wagonjwa wataenda Mwananyamala, wataenda Amana, wataenda kwenye vituo vya afya 350 ambavyo Serikali imeviboresha ili kuviwezesha kutoa huduma. Nitoe wito kwa wanawake, Muhimbili ni National Hospital sio mtu yoyote unaenda tu kwa ajili ya chek up.

Mheshimiwa Spika, suala la pili anataka partition, Mheshimiwa Mbunge angetembelea vituo vya afya tunavyojenga, asingeuliza hili swali, tunajenga kwa kuhakikisha tumeweka partition kwa vituo vya afya vyote. Lengo letu sisi anachosema ufaragha, tunafikiria iliwezekana hata baba amsindikize mama anapotaka kwenda kujifungua. Kwa hiyo tumeliona kama Wizara na tumeweka partition zenye staha katika vituo vya afya.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa ni zaidi ya miaka 15 wananchi wa Segerea kupitia hiyo barabara ya Majumba Sita, Sitakishari wamekuwa wanapitia hiyo adha ya kukosa daraja, lakini ni kiungo kikubwa cha Gereza la Segerea, Seminari na sekondari mbalimbali: Je, Serikali haioni ni wakati sahihi wa kutengeneza hilo daraja ili kuondokana na hiyo adha?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Changamoto ya madaraja katika kata mbalimbali za Jimbo la Segerea ni kubwa, nikianzia na Kata ya Tabata, Segerea, Kimanga na nyingine: Je, nini kauli ya Serikali kuondoa hii adha ukizingatia kwamba hili eneo letu halina barabara nyingi za lami na halina mitaro ili kuondoa adha inayowakabili wananchi wetu? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kumbukumbu zangu naamini ziko sahihi kwamba ni mara ya tatu Mheshimiwa Anatropia anaulizia barabara hii. Naomba nichukue fursa hii kumpongeza kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia kuhakikisha kwamba barabara hii inajengwa.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimejibu katika swali langu la msingi, changamoto ambayo tunakutana nayo kuhusiana na daraja hilo ni namna ambavyo mto unapanuka. Pia naomba yeye pamoja na Wabunge wote wanaotoka Dar es Salaam niwape maneno ya faraja kwamba ndani ya mwezi huu tumeweza kusaini kandarasi ya jumla ya shilingi bilioni 260 ambayo pia inashughulikia na adha ambayo inatokana na mafuriko mvua zinaponyesha na maeneo mengi ya Dar es Salaam yatakuwa yanafaidika katika hilo. Naamini hata hili suala la mto kupanuka baada ya kwamba kingo zimejengwa, adha itapungua.

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuiamini Serikali maana yeye mwenyewe anashuhudia jitihada zinafanyika.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, ameongelea madaraja mengi. Naamini katika package ya shilingi bilioni 260 nayo itakuwa imekuwa covered. Kama haitoshi, tumeweza kuweka taa 5,000 ndani ya Mji wa Dar es Salaam kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wanaendelea kufaidi matunda ya chama chao.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni wiki iliyopita tu tumepta taarifa ya kuvuja kwa bomba la gesi, suala ambalo ni la hatari lakini ni kudra za Mwenyezi Mungu hakuna madhara yaliyojitokeza. Sasa licha ya juhudi za Serikali kuunganisha viwanda na gesi, nini hatua wanazochukua kunusuru hali ya namna hiyo isijitokeze kwa ajili ya kunusuru maisha ya wat? Swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; katika utawala wa Awamu ya Nne kazi kubwa ilifanyika ya kuhakikisha gesi inazalishwa na kusambazwa viwandani kama njia au nishati mbadala, lakini kwa sasa tunaona nguvu kubwa imewekwa kwenye Stiegler’s na miradi mingine ya umeme wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali; Kwa kuwa mradi wa gesi ulikuwa haujatumika kwa asilimia mia moja na tunaona tumehamia mradi mwingine, ni nini mkakati uliopo kuhakikisha mradi wa gesi unazalishwa na unatumika kwanza katika full capacity kabla ya kuhamia miradi mingine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Anatropia katika swali lake la kwanza ameeleza namna ambavyo taarifa ilitolewa rasmi na TPDC kuhusu kuvuja kwa gesi kwenye maeneo ya Somanga Fungu. Kama anavyofahamu tangu imeanza kujengwa miundombinu ya gesi, tangu gesi imeanza kutumika kwa mara ya kwanza 2004 mpaka sasa ni tukio la kwanza. Kwa hiyo, ni wazi kabisa miundombinu iliyojenga taratibu zote za precaution juu ya masuala ya bomba yalizingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, taarifa rasmi imetolewa, wataalam wa SONGAs wakishirikiana na TPDC na Wizara ya Nishati walikuwa eneo la tukio na kila kitu kilifanyiwa kazi na kwa sasa kwa kweli hali imetengamaa na tutaendelea kuchukua hatua stahiki kuhakikisha kwamba matukio kama haya hayajitokezi na kama ambavyo inaonesha ni mara ya kwanza. Kwa hiyo, nataka nimtaarifu kwamba hatua zote zitachukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameulizia namna gani tutaendelea kuwekeza katika miradi ya gesi na amehusisha kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imejielekeza kwenye mradi wa Mwalimu Nyerere Hydro Power. Naomba nimtaarifu Mheshimiwa Anatropia kwamba katika suala zima la uwekezaji wa masuala ya nishati hususan ya umeme, vipo vyanzo mbalimbali; Serikali yoyote lazima itumie vyanzo mbalimbali mbadala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaposema masuala ya gesi, umeme wa maji, umeme wa makaa ya mawe, umeme wa upepo na umeme wa nishati mbadala pia. Kwa hiyo, Serikali ilipoamua kujielekeza kwenye mradi huu wa Mwalimu Nyerere Hydro Power, ni kuhakikisha kwamba lengo la uzalishaji wa megawatt 10,000 ifikapo 2025 linafikiwa kwa mradi huu mkubwa ambao utazalisha megawatt 2,115.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumepata kusema ndani ya Bunge chanzo hiki cha kuzalisha umeme wa maji kina nafuu, kinagharimu shilingi 36 tu kwa unit, lakini pia Serikali inaendelea na uwekezaji wa miradi ya kuzalisha umeme kwa gesi. Kwa mfano, hata sasa hivi kuna mradi wa kuzalisha umeme wa gesi Mtwara wa Megawatt 300 lakini pia upo Mradi wa Somanga Fungu Megawatt 330.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara nchini Japan, aliambatana na Maafisa kutoka TPDC akiwepo Mkurugenzi Mtendaji lakini pia hivi karibuni ametoka Urusi, kote kule wamezungumza na wawekezaji mbalimbali na amewaalika kwa niaba ya Serikali kuja nchini Tanzania hapa kuwekeza katika miradi ya gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kujielekeza kwenye miradi ya gesi na miradi mingine yoyote ili kupata energy mix ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba niseme, taarifa za soko kukamilika kwa asilimia 50 siyo kweli, labda tuambiwe 20 mpaka 30, lakini pia soko hilo limesimama kuendelezwa tangu mwaka 2013. Swali la hivyo lilijitokeza Bungeni mwaka 2016 na taarifa iliyotoka ni kwamba, Nkwenda ilitengewa shilingi milioni 385….

MWENYEKITI: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, najenga hoja, lakini pointi yangu ni kwamba, kumekuwepo na taarifa za kutenga fedha tangu mwaka 2016/2017 ambazo hazijaenda. Sasa swali, hizo bilioni 2.5 kama tumeahidiwa muda mrefu na hazijaenda, zitakwenda kweli?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Wilaya ya Kyerwa iko mpakani, inapata faida ya kuwa na Rwanda na Uganda, hakukuwa na juhudi zozote za kujenga viwanda na kuifanya wilaya kuwa damping place ya bidhaa kutoka Uganda. Nini mkakati wa Wizara kujenga viwanda katika wilaya hii ili kuifungua?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli kama alivyokiri kwamba swali hili lilishawahi pia kuulizwa na Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Mbunge wa Jimbo hilo na msisitizo wetu ni uleule, kwamba Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Kilimo na Serikali kwa ujumla, pamoja na Waheshimiwa Wabunge, ni kwamba tunayo dhamira ya dhati, kuhakikisha kwamba, masoko haya ya mpakani yanaimarishwa, ikizingatiwa kwamba hiyo ni sehemu ya kuondoa vikwazo kwa wafanyabiashara wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakumbuka kwamba tarehe 6 Septemba, 2019 Marais wetu, kutoka Uganda pamoja na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, walifanya mkutano kupitia Baraza la Biashara wa kuimarisha biashara za mipakani. Kwa hiyo, suala hilo ni la kipaumbele na litafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusiana na kujenda viwanda, hiyo ni moja ya fursa ambazo ziliibuliwa katika kongamano hilo la wafanyabiashara na nimhakikishie tu kwamba, kadri muda unavyoenda, hayo yote yatashughulikiwa kwa nia ya kuongeza tija ya bidhaa zetu na kuhakikisha kwamba wananchi wetu wa Afrika Mashariki na Tanzania wanafaidika kwa pamoja.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Wazir, licha ya hayo majibu kwamba, vyuo vipo bado hawa wataalam wanaokuwa wanamaliza kwenye vyuo hawapewi ajira na ndio maana tunazidi kuona upungufu wa maafisa ugani kwenye maeneo yetu. Je, nini mkakati wa Serikali kuajiri maafisa ugani wa kutosha kwa ajili ya kusaidia kufundisha wakulima kuzalisha mbegu bora?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Mkoa wa Kagera hususan Wilaya ya Kyerwa ni walimaji wakubwa wa zao la mgomba, kwa maana ya migomba. Nini mkakati wa Serikali kuja na viwanda au kuja na mbinu ya kuongeza thamani katika zao la ndizi kwa kuwa hilo zao au ndizi huwa zinaharibika muda mfupi baada ya kukomaa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza anataka kujua mkakati wa Serikali kutoa ajira kwa maafisa ugani; kwanza niseme ni kweli maafisa ugani hawatoshelezi, lakini kwamba, tutaendelea kuajiri kutokana na vilevile kuzingatia kipato cha Serikali kwa sababu hata tukiwaajiri hawa wana stahiki zao lazima wapewe, badala yake tukija kuwaajiri bila kuwalipa tutaanzisha changamoto nyingine ambayo haiwezekani. Kwa hiyo, tutaendelea kuajiri kwa kuzingatia uwezo wa serikali kuwalipa na kutoa gharama nyingine. Lakini la katika kukabiliana na tatizo lililopo kama Serikali cha kwanza mkakati tuliokuwanao tunaendelea kujenga vituo vya rasilimali kilimo kila kata, ili maafisa ugani wachache hawa waliokuwepo waweze kuwakusanya wakulima na kutoa elimu ya kilimo cha kisasa kwa wakulima walio wengi kwenye kata zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwenye suala la Kagera kwenye suala la migomba; ni kweli migomba ni zao ambalo linapoteza thamani mapema. Mkakati wa Serikali kama tulivyosema siku zote Serikali ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali ya Viwanda, tutaendelea kuweka mazingira ya kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje ili kuja kuwekeza katika viwanda kuongeza thamani. Na hii tutumieni kama fursa hata wabunge tuna uwezo hapa wa kwenda kuanzisha hivi viwanda vidogovidogo kuongeza thamani kwa sababu Serikali tulishajitoa kwenye suala la kufanya biashara tangu miaka ya 90.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nitoe masikitiko kwamba leo ni mara ya nne ninauliza swali kuhusu kulipwa fidia kwa wananchi wa Kipunguni. Leo najibiwa kwa mara ya nne, mara ya tatu majibu yalibadilika nikaambiwa wangelipwa kwa mwaka wa fedha ulioisha, lakini kwa jibu la leo naona tumerudi nyuma. Serikali inasema watalipwa pale itakapopata fedha, sio sahihi kabisa hawa wananchi wamezuiwa kuendeleza maeneo yao kwa muda mrefu. Wananchi wengi wanakufa, wengine wanashindwa kujiletea maendeleo ni changamoto kubwa sana. Sasa swali langu halijajibiwa ni lini hawa wananchi watalipwa fidia kwa kuwa tuliambiwa wangelipwa mwaka jana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili zaidi ya wananchi 322 walienda mahakamani baada ya kutoridhishwa na mchakato ambao ulikuwa ni pamoja na kutolipwa viwango stahili na kutokubalina na tathimini.

Sasa Serikali ipo tayari kurudi na kuongea na wananchi hawa waondoe kesi mahakamani wafanyiwe tadhimini upya ili walipwe stahili zao sambamba na tathimini ya sasa ili wapate faida ya maeneo yao? Naomba majibu.
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mbunge Anatropia kuhusiana na fidia ya Ukonga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nitajibu swali la mwisho, suala la mahakamani kwa sababu wao wameenda mahakamani hatuwezi kulizungumza humu Bungeni. Niombe Mheshimiwa Mbunge tuache hatua za kimahakama ziendelee, ruling inatakapokuwa imekuja basi sisi ndio tutaendelea nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu fidia ndio utaratibu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inalipa fidia pale ambapo inatekeleza mradi. Awamu ya kwanza tulikuwa tunajenga Terminal III tulilipa fidia kupata lile eneo na ukuta tumejenga. Tutakapohitaji kufanya maendelezo ya ule mradi tena kama ambavyo jibu la msingi limesema basi tutaendelea, tutachukua hilo eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ni kweli kwamba tumezuia wananchi wasifanye maendelezo katika eneo ambalo tumeli-earmark kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. Na hilo sio kwenye uwanja tu hata kwenye barabara. Kwa hiyo, tunafanya hivyo ili serikali pia isiingie gharama kubwa wakati wa ujenzi wa barabara wakati wa fidia.

Kwa hiyo, nikujibu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi ipo makini itahakikisha kwamba pale ambapo inatekeleza mradi watalipwa fidia kwa mujibu wa sheria.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya Serikali kuahidi kwamba inaenda kujenga jengo hilo la Mahakama ya Wilaya katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020, bado Mahakama ya Bariadi inapitia changamoto ya upungufu wa Mahakimu, hivyo kusababisha kesi nyingi kuchelewa: Je, Serikali ina mpango gani kwa wakati huu mfupi kuisaidia Mahakama ya Bariadi ili iweze kukidhi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wakati wananchi wa Itilima wanatembea kilometa 37, wenzao wa Wilaya ya Kyerwa wanatembea zaidi ya kilometa 100. Wananchi wa Murongo, Kaisho, Bugomora, Bugara, wanatembea umbali mrefu kufuata hiyo huduma katika Mahakama iliyoko Wilaya ya jirani…

MWENYEKITI: Swali! Uliza swali!

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali. Ni mkakati gani wa muda mfupi kuwasaidia wananchi wa Kyerwa waweze kupata huduma katika wilaya yao kabla ya kufikia mwaka 2019/2020. Nakushukuru. (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza kutoka kwa Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ya Bariadi inafanya kazi nzuri sana. Hivi karibuni nilipitia kule na nikaona msongamano wa kesi mbalimbali. Ni moja ya majukumu makubwa ya Wizara hii, siyo tu kujenga Mahakama katika ngazi mbalimbali, lakini kutoa mafunzo kwa Mahakimu kadri ujenzi unavyoendelea. Hii inaenda sambamba na kuwasaidia wananchi kwa kuwapa haki ya kusimamia mashauri yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili. Mahakama ya Wilaya ya Kyerwa inahitaji kupata Mahakama yake mara moja. Katika mpango wa Mahakama ya Tanzania kama nilivyoeleza siyo tu tunataka kuleta Mahakama karibu na wananchi, lakini kuhakikisha kwamba tunapunguza kero ambazo wananchi wanapata ili kupata haki yao na kwa wakati. Kutokana na mkakati huo, tutaendelea kusomesha Mahakimu katika ngazi mbalimbali na tutaendelea kupanua ujenzi wa Mahakama katika ngazi mbalimbali hasa katika wilaya hiyo ambayo Mheshimiwa umeizungumzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wanaozalisha umeme ni TANESCO na wanaopanga bei ya kuuza umeme ni EWURA. Kwa muda mrefu TANESCO imekuwa haipati faida, katika kipindi cha miaka kumi iliyopita ni mwaka 2008 na mwaka 2014 waliweza kuzalisha bila hasara.

Je, Serikali haioni ni wakati muafaka kuwa inatoa ruzuku ya upungufu wa gharama katika uzalishaji wa umeme pale ambapo TANESCO wanakuwa hawapati faida kutokana na mauzo yao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; wanunuzi wa umeme wanaoomba kuunganishiwa umeme wakati mwingine hulazimika kununua nguzo na pale maeneo ambako mpango wa Serikali haujaanza, wamekuwa wakitumia kuanzia 500,000 mpaka milioni kununua nguzo lakini nguzo zinabaki kuwa mali ya TANESCO.

Kwa nini wale wanaojinunulia nguzo na kuunganishwa wasiwe wanapewa units za umeme sambamba na ile gharama waliyotumia kununua nguzo ambazo ni mali ya TANESCO? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. kimsingi Shirika la Umeme TANESCO ni Shirika la Serikali na kwa kweli kwa mara nyingi sana ingekuwa limeachiwa lijiendeshe lenyewe bila kusaidiwa kabisa na Serikali labda sasa hivi lingekuwa limefungwa. Lakini kwa kutambua kwamba hilo ni shirika pekee ambalo pia linachochea uchumi katika nchi yetu kwa maendeleo ya Watanzania kwa ujumla, Serikali yenyewe imekuwa pia ikitoa fedha kwa ajili ya kulisaidia shirika hili pamoja na misaada mbalimbali ikiwemo ya kuanzisha vituo vya kuzalishia umeme, kurekebisha mifumo kwa mfano kujenga line ya msongo wa kv 400 ambao unatoa Iringa mpaka kwenda Mwanza, na sasa hivi unategemea tena kujengwa mwingine wa kv 400 kutoka Iringa mpaka Mbeya, Tunduma, Sumbawanga, Mpanda, Kigoma ambayo ni 400 na kutoka pale kv 220 kwenda mpaka Nyakanazi.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuanzisha uzalishaji katika maporomoko ya maeneo mbalimbali. Kwa hiyo, Serikali imekuwa ikitoa ruzuku ya aina mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili kuhusiana na kwa nini mwananchi anapokuwa amelipishwa nguzo hiyo nguzo inatakiwa iwe ni mali ya TANESCO; sio nguzo tu, hata transfoma, akifungiwa transfoma ambalo amelinunua mwenyewe bado anashauriwa kuwa ni mali ya TANESCO. Kuna faida kubwa sana kwa kufanya hivyo kwa sababu nguzo ikishakuwa imejengwa pale utatumia lakini ikitokea imeoza kama umeshairejesha kuwa ni mali ya TANESCO inakusaidia kwamba hata wewe usiweze tena kununua nguzo, ile kazi ya ukarabati inafanyika na TANESCO.

Mheshimiwa Spika, lakini siyo hivyo tu, pale nguzo inapokuwa imefika maeneo hayo inawezesha pia kumfanya mwananchi mwingine aweze kuunganishiwa ikizingatiwa kwamba hatuwezi kuweka nguzo nyingi katika mtaa mmoja. Ileile line moja inayokuwa imenda inasaidia na hata hivyo hizo bei zinakuwa siyo bei kamili, zinakuwa zimezingatia sana kumfanya mwananchi aweze kununua kwa bei anayoimudu.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa muda mrefu baadhi ya vituo vya mahabusu, mahabusu wamekuwa wakitumia ndoo kama sehemu ya kujihifadhia wanavyokuwa mle ndani kwenye hivyo vituo. Je, kutumia hivyo vindoo ni sehemu ya adhabu? Kwa sababu imekuwa si tu inadhalilisha watu bali ni kukiuka haki za binadamu.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie kwamba kwa kiwango kikubwa matumizi ya ndoo yanapungua na nina takwimu baadaYe nimpatie zinazoonesha kwmaba tumefanya jitihada za kutosha kupunguza matumizi ya ndoo kwa maana ya kuongeza ujenzi vya vyombo katika magereza yetu na kwa hakika kwa kasi hii ambayo tunaenda nayo basi miaka si mingi sana tutaondokana kabisa na tatizo hili la matumizi ya ndoo katika magereza.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Swali la kwanza, Serikali imekiri kwamba matukio ya kujifungua watoto njiti au mtoto zaidi ya mmoja hayakuwa makubwa hapo awali ila tunaongea kujifungua watoto njiti na mtoto zaidi ya mmoja ni matukio ambayo yamezidi kuongezeka.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kutengeneza kanuni ya kuongeza siku kwa familia ambayo inapata hususan watoto njiti au watoto zaidi ya mmoja kwa sababu changamoto yake ni kubwa badala ya kuacha ilivyo leo inakuwa kama amnesty ya kupewa hiyo nafasi ya kulea hao watoto? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa wanaume ni kiungo muhimu katika familia na hasa familia inavyopitia changamoto ya kupata watoto njiti au watoto zaidi ya mmoja. Serikali haioni umuhimu pia wa kubadilisha kanuni ya kumruhusu mwanaume kukaa nyumbani kusaidiana na familia kwa si chini ya zaidi ya wiki mbili mpaka tatu ukizingatia kwamba hiyo likizo inatolewa mara moja kwa miaka mitatu ili akaisaidie familia pia? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya mdogo wangu Mheshimiwa Anatropia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana kwa kuona umuhimu wa maternity na paternity kwa watumishi wa Umma. Hata hivyo, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi ni kwamba katika kile kifungu cha Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma cha 12(3) kama Serikali tumeongezea siku 14 zaidi kwa wale wamama wote wazazi ambao wanajifungua watoto ya wawili.

Mheshimiwa Spika, hii ni kuonesha umuhimu kwa mama mzazi kwa sababu sote humu ndani ni wanawake na wanaume, tumezaliwa tumelelewa na wanawake na tunajua kabisa huyu mama mzazi anapojifungua anakuwa na complications nyingi lakini vilevile ndiyo anayenyonyesha watoto hata afya ya yule mama inahitaji kuimarika. Ndiyo maana kwa msingi huo tumeweza kuongeza siku 14 zaidi kwa mama mzazi huyu ambaye atajifungua watoto zaidi ya wawili.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili kuhusu paternity; vilevile nimeshajibu kwenye jibu langu la msingi kwamba katika kifungu kile cha 13 cha Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma baba mzazi na yeye anatambuliwa kuwa ni baba wa mtoto na ndiyo maana tumetoa kile kifungu kisheria kabisa kwamba angalau siku tano maana siku tano zile za mwanzoni mama akijifungua ndiyo kipindi hatarishi ambacho mama naye anamuhitaji baba awepo nyumbani.

Mheshimiwa Spika, vilevile huyu baba endapo mazingira kutokana na ile familia hayaruhusu, basi anaweza akaomba kibali kutoka kwa Katibu Mkuu Utumishi kupitia kwa mwajiri wake. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara ya Bugeme – Nkwenda – Isingiro mpaka Mrongo yenye urefu wa takribani kilometa 135 ikiunganisha Wilaya ya Kyerwa na Karagwe, lakini Kyerwa na Uganda. Swali, ni lini Serikali itakamilisha, ni lini Serikali itajenga hii barabara kwa kiwango cha lami kwa kuzingatia umuhimu wa hiyo barabara na hasa wakazi…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Anatropia swali lako lilivyoisha nilikuwa nimekata maneno. Kwa hiyo, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, majibu.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge ambaye ameelezea barabara yenye urefu wa kilometa 135 ambayo ni ya Kyerwa – Karagwe, lakini pia inakwenda Uganda:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika swali la nyongeza Mheshimiwa Rais amesema atakapokuwa anakamilisha barabara zote za kilometa 2,500 na kilometa 6,006 tutakuwa tumeunganisha wilaya zote za Tanzania kwa kiwango cha lami, mikoa yote ya Tanzania kwa kiwango cha lami, lakini pia na barabara kuu zote (trunk roads) ambazo zinaunganisha nchi na nchi kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimpe uhakika Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza kwamba, barabara hiyo ni kati ya barabara ambazo zitatekelezwa. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kyerwa kuna changamoto kubwa ya maji na hasa Kata za Kibale, Bugomora na Mrongo ila ninavyoongea hapa Kijiji cha Mgorogoro kuna tanki kubwa la maji ambalo tangu limewekwa…

SPIKA: Ni wapi huko unakokuulizia?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Kata ya Kibale.

SPIKA: Kata hiyo iko kwenye Wilaya gani?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kyerwa, Jimbo la Kyerwa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tanki limewekwa kama urembo halijawahi kutoa maji. Kila siku wananchi wakiona habari za maji wananitumia message na sasa wamenikumbusha. Ni lini lile tanki katika Kijiji cha Mgorogoro litaanza kutoa maji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia kuhusu tenki kubwa lililokamilika lakini halitoi maji. Mkakati wa Wizara ni kuona kwamba miradi hii ambayo miundombinu imekamilika kufikia mwezi wa tatu kwenye Wiki ya Maji tunataka kuona kwamba maji yanatoka.

Mheshimiwa Spika, nimuahidi Mheshimiwa Anatropia kwamba nitafika huko Kyerwa na kuona nini kinasababisha maji hayatoki. Lengo ni kuona kwamba maji yanapatikana bombani. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Niweke kumbukumbu sahihi, siyo kweli kwamba wamemaliza kulipa vyama vyote; kuna AMCOS ya Rumulo ikiunganisha Vijiji vya Rugasha, Kibingo na Mrongo wamelipwa nusu ya malipo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza. Changamoto kubwa ambayo wakulima wanakutana nayo inayotokana na Vyama vya Ushirika ni kushindwa kuwapa fedha kwa wakati na sababu ni kwamba fedha inakopwa benki kwa asilimia 9. Serikali haioni ni wakati muafaka kwa benki za kilimo kupunguza riba kwenda mpaka asilimia 5, ili waweze kupata uwezo wa kulipa kiasi cha kutosha cha kahawa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa, sasa tunafanya biashara huru kwa kilimo na biashara nyingine ikiwa ni sera ya Serikali. Nchi jirani kama Uganda wananunua kahawa kwa gharama au kwa bei nzuri. Ni kwa nini Serikali isitengeneze special arrangements kwa wakulima hata wa Kagera waweze kuuza kwa makampuni ya Uganda ambayo yanatoa bei iliyo nzuri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nitashukuru akinipa facts za kwamba Chama cha Msingi alichokitaja hakijalipwa kwa sababu takwimu tulizonazo Wizarani na fedha zilizotolewa na TADB kwa ajili ya kulipa wakulima wa Mkoa wa Kagera tumelipa 100%. Kwa hiyo, kama kuna kiongozi yeyote wa Chama cha Msingi ama Chama Kikuu cha Ushirika hajafikisha fedha kwa wakulima hao, tutachukua hatua immediately kwa sababu ni uhujumu uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la bei ya Uganda; mwaka huu katika Ukanda huu wa Afrika Mashariki, ukitoa wakulima walioko katika nchi ya Rwanda ambao wana mkataba maalum na Starbucks ambapo sisi kama Serikali sasa hivi tumeanza maongezi nao kwa ajili ya kununua moja kwa moja kutoka kwa wakulima, wakulima wa Mkoa wa Kagera wameuza bei nzuri kuliko mkulima wa Uganda. Kama mna bei na facts kwamba kuna mnunuzi Uganda anatoa bei nzuri kuliko mnunuzi wa Tanzania, milango ya Wizara ya Kilimo iko wazi, karibuni mtuletee. Hata hivyo hatutaruhusu biashara isiyokuwa na contract; yenye clarity ya mambo mawili (bei na volume) kuliko kuwaambia wakulima kwamba tutanunua na mchezo wa butura umekuwa ukiendelea. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, hatutaruhusu mkulima kufuatwa shambani kununuliwa kahawa. Mheshimiwa Mbunge wewe ni mzoefu, Kagera kumekuwa na biashara inaitwa butura na biashara hii imekuwa ikisimamiwa na viongozi wenye mamlaka na nguvu ambao wamekuwa wakienda kununua kahawa kwa wakulima kwa Sh.500 na Sh.700 hatuwezi kuruhusu. Kama kuna tatizo la malipo katika Vyama vya Msingi, tushughulikie tatizo la ucheleweshaji wa malipo na wala siyo kuua mfumo tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la riba, mpaka sasa kupitia Tanzania Agricultural Bank ndiyo imekuwa benki ambayo imeshiriki katika kushusha riba kwa wakulima ambao wamekopa katika benki mbalimbali. Walianza na riba ya asilimia 11 Vyama vya Ushirika vya Kagera sasa hivi wamepewa kwa riba ya asilimia tisa.

Vilevile commercial banks zilikuwa zinawapa riba kwa asilimia 20 kwa guarantee ya kupitia TADB, mikopo hiyo wamekuwa wakipewa kati ya asilimia 13. Tumeanza mazungumzo na commercial bank ili riba katika sekta ya kilimo isizidi asilimia 10. Majadiliano haya yameanza na tunaamini tutafikia lengo hili kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wakulima wanapata mikopo yenye riba nafuu.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati DKt. John Pombe Magufuli, alivyokuwa Karagwe aliahidi kwamba watu wa Kyerwa watajengewa barabara kilomita 50 kwa lami. Hii barabara ya lami inahitajika kweli kwa sababu imekuwa ni mgogoro wa wananchi, je, itaanzia wapi hiyo kilomita 50 ya lami? Licha ya kuahidiwa bado ujenzi huo haujaanza. Swali, ni lini hizo kilometa 50 tulizoahidiwa na Mheshimiwa Rais zitaanza kujengwa hata ikibidi tukaongezewa zikawa hata 100? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ahadi zote za Viongozi wa Kitaifa tunazizingatia na huwa tunazitekeleza. Ahadi ikishatolewa kuanza kwa barabara si kuingia site na kuona magreda yanaanza kutembea lakini barabara itafanyiwa usanifu na usanifu wa kina ndipo itakapoanza kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la pili barabara itaanzia kujengwa wapi, sisi kama Serikali kokote tukianzia ili mradi kilomita 50 zitatimia tutaijenga barabara hiyo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea na taratibu za kutimiza ahadi za Viongozi wa Kitaifa ikiwa ni pamoja na barabara hii ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja kwamba zitajengwa kama zilivyoahidiwa na Kiongozi wetu wa Kitaifa. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Katika majibu aliyotoa Naibu Waziri, anaeleza mifumo yote ya ununuzi inahusisha kukusanya kahawa katika maghala kwa sababu moja tu ya kuzuia butura. Serikali kushindwa kuzuia butura na kuleta sababu ya kukusanya kupitia maghala ni kutesa wakulima.

SPIKA: Butura ndiyo nini?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, butura ni mfumo ambao wafanyabiashara wanakwenda kwa wakulima kabla ya msimu wanawapa fedha halafu baadaye msimu ukifika wanawapa kahawa.

SPIKA: Ni kama kwenye korosho kangomba.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, sawa. Wamekuwa wakifanya hivyo siyo kwa sababu wanapenda, kwa sababu hela ya kahawa inaletwa ikiwa imechelewa. Sasa nataka niulize swali; ni kwa nini Serikali inapata kigugumizi kuruhusu wafanyabiashara wakanunua moja kwa moja na Serikali ikasimamia kuzuia butura? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama Serikali ikiruhusu KDCU au vyama vya ushirika kukusanya kahawa ije sasa na mkakati wa kuwawezesha kupata fedha ili walipe wakulima mwanzoni mwa msimu kwa sababu inahitajika fedha kwa ajili ya kuandaa mashamba; katikati ya msimu inahitajika fedha kuvuna kahawa na baadaye mwishoni wakiwa wamemaliza kuuza. Nataka nijue Serikali imejipangaje kuhakikisha wakulima wanapata fedha katika awamu tatu na siyo kusubiria baadaye kama wanavyofanya sasa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba iingie tu on record vilevile concern ya Wabunge wote wa Mkoa wa Kagera katika ku- perfect mfumo wa ulipaji ni concern genuine ambayo tunaifanyia kazi kama Serikali. Hata hivyo, niseme kitu kimoja; mfumo wa ushirika ni basic principle ambayo kwanza imeelekezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, pili, ndiyo mfumo sahihi wa aggregation kwa wakulima wadogowadogo unaoweza kuwalinda. Kwa hiyo, kuondoa mfumo wa ushirika tutakuwa tunatenda dhambi kubwa kabisa ya kuwalinda wakulima wadogowadogo. Tunachotakiwa kufanya ni ku-perfect na tumefanya hivyo katika Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera, Chama cha KDCU na Chama cha KCU katika kipindi cha miaka miwili hii ndiyo vyama pekee ambavyo tumevipatia fedha kupitia Benki ya Maendeleo ya Wakulima kwa riba isiyozidi asilimia tisa. Tunaelewa kuna tatizo la ucheleweshaji wa malipo lakini hatuwezi kufananisha tatizo lililokuwepo miaka miwli iliyopita na msimu huu. Tuwe wakweli na tuseme ukweli mbele ya Mwenyezi Mungu. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, kuhusu wanunuzi kwenda kwa wakulima moja kwa moja; hatumkatalii mfanyabiashara yeyote anayetaka kununua kahawa ya wakulima lakini hatutamruhusu kwenda kumpa mkulima wakati ana shida ya hela kwa shilingi 200 halafu aende akaivune kahawa ikiwa haijakomaa. Wanataka kununua kahawa, waje na leo mimi nina kikao na wewe Mheshimiwa Mbunge nakukaribisha, tutakuwa na kikao cha kahawa tunajadili mfumo na tutawapa leseni mapema. Waseme wazi wanataka kununua kahawa ya wakulima kwa bei gani na volume gani, tutawapeleka kwenye vyama vya msingi lakini direct kwenda shambani hatutaruhusu hilo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Changamoto ya wananchi wa Singida ni sawa na changamoto wanayopitia watu wa Kyerwa na hasa Kata ya Songambele, eneo la Kitebe ambalo wanazalisha sana mahindi lakini kuna changamoto ya barabara tangu lile eneo limekuwepo kwenye Kijiji cha Kitega. Nataka kupata commitment ya Serikali kuhakikisha wanaiunganisha hiyo Kitega na Kata nzima ya Songambele ili tuweze kufanya biashara na Jimbo la Karagwe lakini pia na Rwanda kwa sababu ni mpakani mwa Rwanda pia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali tunatambua mchango mkubwa ambao wamekuwa wakiutoa, tunatambua umuhimu wa barabara zote nchini na ndiyo maana tunaendelea kuongeza fedha na tumekuwa tukizitenga ili kuhakikisha kwamba tunazitengeneza na zinapitika. Hata wananchi wa Kitega katika hiyo Kata ya Songembele tutahakikisha tunawaunganisha ili kuwaondolea hiyo adha ambayo ina wakabili. Kwa hiyo, tutatafuta fedha ili tuzipeleke katika eneo husika. Ahsante sana.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa haya masoko yamesimama muda mrefu, kuanzia mwaka 2013 na maelezo ya Serikali kila siku ni wanatenga bajeti: Sasa swali, Kwa kuwa haya masoko ni strategic, Serikali haioni ni umuhimu wa kushirikisha wadau binafsi katika kuendeleza haya masoko? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali imesema tangu mwaka 2019/2020 kwamba itatenga shilingi bilioni 2.9 kujenga hayo masoko, nataka commitment ya haya masoko kuanza kujengwa.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ni kweli ujenzi wa masoko haya umesimama kwa muda mrefu tangu mwaka 2013/2014 wa mwaka wa fedha huo, kama nilivyosema katika jibu la msingi kwamba ilitokana na changamoto za ufinyu wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mbunge wa Jimbo la Kyerwa, Mheshimiwa Innocent Bilakwate, ambaye amekuwa akiendelea kufuatia sana ujenzi wa masoko haya kwa muda mrefu na ndiyo maana tumesema tunatafuta wadau wengine ikiwemo na benki, lakini na wadau wengine ambao tulikuwa tunashirikiana nao katika kujenga masoko hayo na ndiyo maana mwaka wa fedha huu 2021/2022 unaokuja Serikali imetenga angalau shilingi milioni 500. Lengo ni kukamilisha ujenzi wa masoko hayo.

Mheshimiwa Spika, pili, ni kweli commitment ya Serikali ni kuhakikisha tunajenga masoko ya kimkakati ya mipakani kwa sababu tunajua lengo la Serikali sasa ni kuanza ku-access masoko ya nje baada ya bidhaa nyingi au mazao mengi ya kilimo Tanzania kuongezeka. Kwa hiyo, ni lazima tutafute masoko ya nje. Kwa hiyo, ni mpango mkakati wa Serikali kuhakikisha tunajenga masoko ya mpakani, lakini ku-access masoko ya nje kupitia fursa mbalimbali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, katika siku za hivi karibuni tumeshuhudia kuona wasomi, wahadhiri, maprofesa wakiondoka katika taasisi za kufundisha na kuingia katika utumishi mwingine tofauti.

Je, upi umekuwa mkakati wa Serikali kama succession plan kwamba ikimuondoa profesa fulani mwenye uzoefu fulani katika chuo anaweza kuwa replaced ili kuondoa lile pengo ambalo linakuwa linajitokeza?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, ndani ya Serikali na hasa kupitia Sheria za Utumishi wa Umma ipo mipango ya succession plan kuhakikisha kwamba ikama za utumishi wa umma zinazingatia mahitaji tuliyonayo nchini.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asiwe na wasiwasi, tutaendelea kusimamia mifumo tuliyoiweka ya kuzingatia na kulinda ikama ya utumishi wa umma nchini ili kuhakikisha kwamba mapungufu hayapatikani pale ambapo wataalam wanahamia katika masuala mengine ya kiutendaji. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, changamoto ya wananchi wa Manonga inafanana sana na wananchi wa Jimbo la Kyerwa. Nimekuwa nikiongelea changamoto ya Kijiji cha Kitega, Kata ya Songambele ambacho kipo chini ya mlima na kipo karibu na Rwanda, hakuna mawasiliano ya Redio wala simu wala kitu chochote. Ni mpango gani wa Serikali na wa dharura kuhakikisha kile Kijiji tunakirudisha Tanzania kwa kukipa mawasiliano kwa sababu ni kama wapo gizani. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali kupitia Wizara yetu na kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote tayari tumeshafanya tathmini katika Vijiji na Kata zote zilizopo mipakani na katika maeneo ya mbuga na hifadhi. Tayari tunaenda kuviingiza katika mpango wa kuhakikisha kwamba mwaka huu tunaenda na utaratibu wa kuanza kwanza na maeneo ya mipakani.

Katika siku ambayo tunapitisha bajeti yetu tuliwaambia Waheshimiwa maeneo ya mipakani ndio ambayo tunaenda kuyapa kipaumbele yakiwepo maeneo ya Mheshimiwa Mbunge, ahsante sana.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa licha ya Kata ya Lukulaijo kuwa jirani na Kata ya Nkwenda ambayo ni mjini bado kuna vijiji viwili ambavyo havina umeme ambayo ni Kijiji cha Mgorogoro lakini na Kijiji cha Mkombozi, nataka nijue commitment ya Serikali kwa sababu vile vijiji havipo mbali; ni lini vitapelekewa umeme?
WAZIRI NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya katika maswali ya nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa Mheshimiwa Anatropia, vijiji vyote na mitaa yote ya mjini pamoja na maeneo ambayo ni Mgorogoro pamoja na Lukulaijo na maeneo mengine ambayo yamebaki tumesha-design mkandarasi wa peri-urban ambaye ataanza kupeleka umeme mwezi ujao, na ndani ya miezi tisa atakamilisha maeneo yote ya kwa Mheshimiwa Mbunge watakuwa wameshapekewa umeme. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, kwa kuwa Naibu Waziri amejibu hapa kwamba, ni Sera ya Serikali kwamba kuwe na zahanati kwa kila kijiji, lakini pia, kituo cha afya kwa kila kata. Wilaya ya Kyerwa yenye kata 24 ina zahanati tatu, yenye vijiji 99 ina zahanati 23. Ningependa kujua je, kwa wilaya ya Kyerwa hiyo sera inatekelezwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni mkakati gani Serikali ilionao kuhakikisha wananchi wa Kyerwa nao wananufaika na Sera ya Serikali ya kuwa na huduma ya afya kila kijiji, kila kata? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge. Kama ambavyo nimejibu katika maswali ya msingi kwamba, Serikali katika kipindi cha miaka mitano imejenga zahanati zaidi ya 1,200 vituo vya afya zaidi ya 488 na hospitali za halmashauri zairi ya 102, lakini mkakati huu unaendelea kutekelezwa na Halmashauri hii ya Kyerwa ni miongoni mwa halmashauri ambazo zitapewa kipaumbele kuhakikisha vijiji vyake na kata zinapata vituo vya afya ili kusogeza huduma za afya kwa wananchi. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, awamu zinazofuata tutaendelea kuongeza kasi, lakini pia kuipa kipaumbele halmashauri ya Kyerwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili. Mkakati wa Serikali ni huo wa kuhakikisha kwamba, sasa kila kijiji, lakini pia kila kata na kila halmashauri inapata vituo vya huduma za afya, ili kusogeza huduma kwa wananchi. Nakushukuru.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Licha ya kutengwa bajeti katika maeneo mbalimbali katika Wilaya ya Kyerwa katika Kata ya Kikukuru haikutengwa hata Shilingi moja; kata hiyo ina vijiji vitatu ambavyo hakuna hata kijiji kimoja chenye maji na wananchi wanatembea umbali wa muda mrefu kutafuta maji.

Sasa nataka kujua ni mpango gani mahususi wa kusaidia hiyo kata ili waweze kujikwamua na wao kupata maji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata hizi alizozitaja katika Jimbo la Kerwa nazo pia zimepewa jicho la kipekee kabisa. Unaweza ukaona kwenye bajeti yetu huku haikupangiwa, lakini kipekee nipende kumshukuru Mheshimiwa Rais ambaye ameweka mkazo katika kuona miradi yote ya maji nchini itafanyiwa kazi. Kama mlivyomsikia, mama yetu ametuahidi kutuongezea fedha zaidi ili miradi yote iweze kutekelezwa. Hivyo nikutoe hofu Mheshimiwa Mbunge, mradi huu pia tutakuja kuutekeleza.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Changamoto ya maji katika Kata za Murongo, Kibale, Bugomora ambazo ni kata za mpakani mwa Mto Kagera zinaweza kumalizwa kama kukianzishwa mradi mkubwa wa maji kutoka Mto Kagera kuja kuhudumia wakazi. Je, ni nini mpango wa Serikali kuhakikisha tunapata maji ya kutosha kutoka Mto Kagera kuhudumia hizi kata ambazo ziko pembezoni mwa huo mto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Anatropia, hakika akina mama tunasemeana vema. Tunafahmu mwanamama ndiye anayepata shida ya kubeba maji kichwani na sisi kama Wizara tumesema lazima tumtue mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji kutoka Mto Kagera sisi kama Wizara ni moja ya vipaumbele vyetu kutumia mito na maziwa makuu kuhakikisha maji yanapatikana. Kama nilivyomjibu Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo, Mheshimiwa Anatropia tutakuja pamoja na Mheshimiwa wa Jimbo tutaweka mambo sawa, Kyerwa maji yatapatikana. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Barabara ya Murongo kuja Kibale kuja Bugara halafu mpaka Mgakorongo ni barabara ya hadhi ya Mkoa. Ikiunganisha Uganda na Tanzania na mchakato wake umechukua muda mrefu. Nataka kujua ni lini hiyo barabara itaanza kujengwa kwa sababu, imekuwepo mchakato wake muda mrefu. Nataka kujua Serikali imejipangaje? (Makofi)
MHE. NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI – (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara iliyotajwa ni barabara kuu na ni barabara ambayo ni kweli inaunganisha Tanzania na Uganda katika lile eneo linaloitwa Murongo. Nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge barabara ile nimeitembelea na barabara hiyo kwa mwaka huu, imetengewa fedha kwa ajili ya kuanza kwa kiwango cha lami ujenzi huo. Kwa hiyo, nimuhakikishie kwamba ipo kwenye mchakato na barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wakulima wa Mkoa wa Kagera kwa muda mrefu wamekabiliwa na changamoto ya mnyauko wa migomba na haikupatiwa ufumbuzi. Hivi sasa kumekuja mnyauko na miche ya kahawa kwa hiyo, mkahawa mkubwa unanyauka. Nataka nipate kauli ya Serikali nini mkakati wao wa kuwasaidia wakulima wa Mkoa wa Kagera na hasa Wilaya ya Kyerwa na Karagwe. Kupambana na changamoto ya kukauka kwa mikahawa yao kutokana na hiyo homa ya virusi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumjibu Mheshimiwa Anatropia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi tu ni kwamba wataalam wa TARI baada ya Wizara kupokea taarifa juu ya athari ya mnyauko wa kahawa, hivi ninavyoongea leo wana zaidi ya siku Saba wako Mkoa wa Kagera kwa ajili ya kufanya utafiti na kuweza kutafuta solution.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisingependa kutoa jibu fupi ambalo halina uhakika hapa, tusubiri wataalam warudi watatupa majibu lakini tunatafuta solution. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa majibu yaliyotolewa, lakini watu wa Kyerwa hawana majikwa asilimia 56 kama Serikali inayoeleza. Changamoto ya upatikanaji wa maji ni kubwa zaidi, naweza kusema ni asilimia kama 25. Kwa hiyo, naomba Serikali ifanye mkakati wa maksudi wa kuwasaidia watu wa Kyerwa wapare maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwamba, ametaja Mradi wa Runyinya, Chanya, Kimuli, Rwanyango, Nyamiaga na Nyakatera ambapo ukiweza kusainiwa na kuanza utapunguza kwa kiwango kikubwa upatikanaji wa maji. Nataka kujua ni lini sasa mkataba utasainiwa kwa sababu imekuwa ni kila siku mkataba unakaribia kusainiwa. Nataka nijue ni lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wananchi wa Kata za Nyakatuntu, Kimuli, Kamuli, Bugara na maeneo mengine wana changamoto kubwa ya maji na wameahidiwa watakuwa kwenye mradi wa vijiji 57 ambapo iwapo utatekelezwa ungepunguza changamoto ya maji. Haujaanza na hatujui unaanza lini. Nataka nijue ni lini huo mradi utaanza na kukamilika ili kuondoa adha kubwa ya maji kwa wananchi wa Jimbo la Kyerwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumpongeza Mheshimiwa Anatropia kwa maswali yake mazuri na ninamwona ana ushirikiano wa karibu sana na Mheshimiwa Bilakwate, Mbunge mwenye Jimbo, ambaye ameendelea kufuatilia miradi hii yote. Mheshimiwa Innocent Bilakwate ni juzi ametoka Ofisini kuhakikisha anaweka sawa miradi hii ambayo inaenda kufanyika katika Jimbo la Kyerwa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tuna mradi wa Kamuli ambao kijiografia upo juu. Tunatarajia mradi huu kwenda kutekelezwa hivi karibuni na utekelezaji wa mradi huu utasaidia kusambaza maji katika vijiji vingi vya Jimbo la Kyerwa. Hivyo, napenda kukutoa hofu Mheshimiwa Mbunge, miradi hii itasainiwa kwa taratibu za Wizara zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, percentage za usambazaji maji katika Jimbo la Kyerwa ni asilimia za kitaalam, siyo za kufikirika kuangalia tu kwa macho na ukasema ni asilimia 20. Ni asilimia zilizotajwa na watalaam, zimefanyiwa kazi na tuna uhakika na kazi tunayoifanya. Nasi Wizara ya Maji siyo wababaishaji, lengo letu kubwa ni kuhakikisha tunamtua ndoo mama kichwani kama ambavyo Mheshimiwa Rais wetu anatutaka. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ujenzi wa barabara ya Mgakorongo kwenda Murongo tathmini imefanyika na wananchi wamekuwa wakisubiri fidia kwa muda mrefu, kiasi kwamba wanashawishika kufanya maendeleo: -

Je, ni lini fidia zitaanza kutoka ili wananchi waweze kuhamia sehemu nyingine waendelee na maisha yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wanaohusika na barabara hii ya kuanzia Omugakarongo, Kigarama hadi Murongo; hii barabara ipo kwenye maandalizi ya kutangazwa zabuni. Barabara hii kabla haijaanzwa tutahakikisha kwamba wananchi hawa kipaumbele ni kuwalipa fidia. Kwa hiyo, kabla hatujaanza kujenga, wananchi kwanza watalipwa fidia na ujenzi wa hiyo barabara utaanza. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; barabara ya Bugene – Itela - Nkwenda mpaka Kaisho ambazo ni ahadi ya Mheshimiwa Hayati Rais Magufuli, kilometa 50. Ni lini barabara hii itaanza kujengwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kutimiza hiyo ahadi.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru: -

Mheshimiwa Spika, ningependa kujua ni lini Serikali itafungua au chuo kikuu au tawi la chuo kikuu Mkoani Kagera kwa kuwa limekuwa ni hitaji la muda mrefu na ukizingatia tuna ardhi ya kutosha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tuna mradi wetu wa heat ambao tunataraji tutaanza kuutekeleza katika mwaka ujao wa fedha, miongoni mwa maeneo ambayo ni focused zone ni katika Mkoa wa Kagera. Kwa hiyo, nikuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge katika maeneo ambayo tunaenda kujenga campus nadhani ilikuweko campus pale ambayo baadae ilikuja kufungwa, tunaenda kuifufua ili kuhakikisha kwamba Mkoa wa Kagera unakwenda kupata chuo hiki.

Vilevile tunafungua chuo kikubwa sana cha VETA katika Mkoa wa Kagera ambapo tunaamini chuo kile kitakuwa na hadhi vilevile ya chuo kikubwa hapa nchini. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, licha ya juhudu za Serikali za kuendelea kukarabati viwanja wa ndege bado vingi vimekuwa vinafanya kazi mchana tu. Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha viwanja vinafanya kazi saa 24?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi viwanja vyote tunapoongelea kiwanja cha Mbeya, kiwanja cha Songwe, kiwanja cha Mtwara, kiwanja cha Msalato, kiwanja cha Geita na hata hivyo viwanja vile tunavyojenga Sumbawanga, Kigoma, Tabora na Shinyanga vyote viko kwenye mpango wa kujengewa taa ili viweze kufanya kazi saa 24 na kazi hiyo inaendelea. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa gharama kubwa huongezeka kutokana kwamba waagizaji wa gesi hufanya binafsi binafsi, kwa maana hakuna bulk procurement: Je, ni mpango gani wa muda mfupi kuhakikisha bulk procurement inaanza kufanya kazi ili kupunguza na kudhibiti gharama ya gesi inayopanda holela? (Makofi)
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kama nilivyozungumza kwenye jibu la msingi, uagizaji mkubwa na uwezo mkubwa wa kuhifadhi na miundombinu ya kupakua na kuhifadhi gesi kwa wingi inasaidia kushusha gharama. Ndiyo maana Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi imeingia makubaliano ya kuongeza uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam kushusha, kupokea na kuhifadhi gesi kwa wingi. Kwa hiyo, Serikali iko mbioni kutekeleza mpango huo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Wananchi wa Kijji cha Kigorogoro Kata ya Kibale kwa muda mrefu walikuwa na changamoto ya maji ya kisima. Kilichimbwa kisima, lakini kilipoanza kutoa maji, yakawa ni maji yenye chumvi kali wananchi wakashindwa kuyatumia. Naomba kuuliza swali: Ni lini wananchi wa Kijiji cha Kigorogoro watachimbiwa kisima kingine ambacho hakina maji ya chumvi, ukizingatia wapo kwenye ukanda wa Mto Kagera? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo ambalo kisima kimechimbwa na maji yakaonekana siyo rafiki kwa matumizi ya binadamu huwa tunayaacha na kutafuta mbadala wake. Ninaamini maeneo hayo watendaji wahusika wanaendelea kutafuta eneo mbadala na maji safi na salama lazima yaweze kuwafikia wananchi wa Kigorogoro.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nataka kujua ni lini Barabara ya Nyakanga kwenda Nyaishozi kuja mpaka Benako itajengwa kwa kiwango cha lami, kwa sababu ni barabara kuu inaunganisha Tanzania na Rwanda?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii tumeshaanza kuijenga kwa kiwango cha lami kilometa 60 na barabara iliyobaki, African Development Bank wako kwenye majadiliano ili kuikamilisha yote kuunganisha Tanzania, Burundi na Rwanda.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Hospitali ya Wilaya ya Kyerwa haina watumishi na hivyo kupelekea wagonjwa wengi kujazana kwenye kituo cha afya cha Nkwenda. Sasa nataka kujua ni lini na ni kwa kipaumbele kiwango gani hiyo hospitali itapewa ili kupunguza adha ambayo kituo cha afya cha Nkwenda inapitia kuwa na wagonjwa wengi.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Theonest Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya Kyerwa ina upungufu wa watumishi pamoja na vituo vingine vya afya, lakini nimpongeze Mheshimiwa Mbunge ambavyo ameendelea kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Kyerwa ambaye mara kwa mara amekuwa anakumbushia kuhusiana na watumishi katika eneo hilo nimhakikishie kwamba tutaipa kipaumbele cha watumishi hospitali ya Wilaya ya Kyerwa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Halmashauri ya Kyerwa ina vituo vya afya Vitatu licha ya kuwa na wakazi zaidi ya 600,000. Napenda kujua tayari kituo cha afya cha Kamuli kimekamilika changamoto imekuwa vifaatiba na Madaktari.

Ni lini madaktari watapelekwa ili hicho kituo kiweze kuongezeka na kusaidia kupunguza adha kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Theonest Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vyote ambavyo vimekamilika na ndio maana jana wakati tunapitisha bajeti hapa tunashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kupitisha bajeti ya Wizara hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo kwa kiasi kikubwa kwenye sekta ya afya tumeweka ununuzi wa vifaatiba pia na ajira za watumishi.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika kituo hiki cha afya katika Halmashauri ya Kyerwa pia tutahakikisha kinapata vifaatiba na watumishi ili kianze kutoa huduma bora zaidi za afya kwa wananchi. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Jiografia ya Jimbo la Kyerwa ni milima na mabonde, hivyo kuhitaji madaraja na barabara kwa maana maeneo mengi hayapitiki. Bajeti ya bilioni mbili haitoshi, nataka kujua commitment ya Serikali ni kwa kiwango gani itaongeza bajeti ili kuweza kusababisha maeneo mengi yafikike?

Mheshimiwa Spika, swali la pili barabara ya Nkwenda- Kakanza-Kimuli mpaka Mabira inatumika na kata zaidi ya 5 na kwa TARURA wamepewa scope ya kilometa tatu ambayo ina urefu wa zaidi ya kilometa 30. Je, ni sahihi kweli kutoa kiwango hiki cha fedha kwa barabara hii nataka kujua mkakati wa dharura kupeleka fedha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Lwehikira Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Anatropia kwa namna ambavyo anashirikiana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Kyerwa Mheshimiwa Innocent Bilakwate na hoja hizi zote ambazo Mheshimiwa Mbunge amezileta Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo amekuwa mara kwa mara anazileta, kwa hiyo niwapongeze kwa ushirikiano huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na fedha kwa maana za madaraja, hali ya milima na mabonde na hali ya mvua tunafahamu na ndio maana Serikali imeendelea kuongeza fedha kutoka bilioni moja mpaka bilioni mbili na milioni mia nane na tisini katika Wilaya ya Kyerwa ili kuhakikisha inaendelea kujenga madaraja, makalveti na barabara. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali itaendelea kuweka jitihada hizo.

Mheshimiwa Spika, hii barabara ambayo inahudumia kata nyingi na inahitaji fedha zaidi ndio maana Serikali imeongeza bajeti na tutaendelea kuongeza bajeti ili tuhakikishe tunafikia kilometa zote 30 ili kata zote ziweze kunufaika. Ahsante sana.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, napenda kujua ni lini Barabara ya Omugakorongo kwenda mpaka Murongo itajengwa ukizingatia Wilaya ya Kyerwa haina lami hata kilometa moja ukiachana na lami ya mchongo ambayo iko Nkwena? Nataka kujua ni lini kwa sababu imechukua muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ya Omugakorongo hadi Murongo tunavyoongea sasa hivi iko kwenye hatua za manunuzi na nina hakika kabla ya kumaliza mwaka huu wa fedha barabara hiyo itakuwa imeanza na nimkumbushe Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itaanza kujengwa upande wa Murongo kuja Omugakorongo ili tuweze kujenga lile Daraja la Mto Kagera ambao unapakanisha sisi na Uganda.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Sheria iko wazi kuzuia mahusiano na mapenzi ya jinsia moja, lakini tunaona kwenye vyombo vya habari watu wakitangaza na kujinasibu kujihusisha na mapenzi ya jinsia moja.

Je, ni hatua kiasi gani zimefanyika kufikishwa Mahakamani ili tuweze kuzibiti kwa mujibu wa sheria? (Makofi)

Swali langu la pili, licha ya kuwepo kwa Sheria bado tumeona utekelezaji wake, pengine utekelezaji ndiyo umesababisha haya tunayoyasema.

Je, ni lini Serikali italeta mabadiliko ya sheria ili kila anayejihusisha, mwenye dalili na mwenye kufikiria aweze

kuchukuliwa hatua ili tuweze kulinda maadili ya nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Theonest kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge amependa kufahamu kwamba makosa hayo yanapojitokeza na watu wakijinasibu hadharani kwenye vyombo kama hatua zimekuwa zikichukuliwa? Hatua zimekuwa zikichukuliwa na ninyi ni mashahidi kwenye Bunge hili tumekuwa tukikemea jambo hili, nitoe rai kwa jamii kwamba jambo hili si la Serikali peke yake ni la jamii kwa umoja wetu ndiyo maana pale zinapokuwa zimebainika tumekuwa tukichukua hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge anahitaji kujua kama tunaweza kufanya marekebisho ya sheria hizi? Sheria hizi zinafanya kazi kuhakikisha kwamba wale wanaobaninika wanachukuliwa hatua na ninyi ni mashahidi ndugu zangu hivi karibuni mahakama zetu zimetoa hukumu kwa watu ambao wamebainika wamefanya hivyo na wamekiri na wamefungwa miaka zaidi ya thelathini. Kwa hiyo, ni jukumu letu sote. Hata hivyo, pale ambapo utafiti utakuwa umefanyika Mheshimiwa Spika alielekeza kwamba utafiti wa kina ufanyike ili matendo haya yakibainika basi tuwe na kauli ya pamoja. Wakati huo ukifika kama marekebisho ya sheria yatahitajika Serikali ipo tayari.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Niabu Waziri kwa majibu. Namwona Mheshimiwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mheshimiwa Nape.

WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kuongeza katika majibu yake mazuri.

Kwanza, hakuna matangazo ya mapenzi ya jinsia moja kwenye main media ambayo yanaruhusiwa na Serikali iko very strictly kwenye hili. Tulikuwa na chanagamoto kwenye online media ambayo mpaka sasa hivi jumla ya tovuti 334, akaunti za Facebook 361, Instagram 168, Twitter 12 na vikoa vya gay zaidi ya 2,456 vimefungiwa kwa sababu ya hatua hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na hatua ambazo Serikali inachukua kufungia baadhi ya hizi online platforms lakini nadhani jambo hili bado liwe ni jukumu la jamii kuchukua hatua kuanzia kwenye familia na kuendelea sasa kwenye maeneo mengine. Nashukuru. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Licha ya wananchi wa Kata ya Kibale, Kijiji cha Kigorogoro, lakini pia Businde na Lukuraijo Mkombozi kukatiwa migomba na mikahawa kwa ajili ya kuwekewa nguzo za umeme, ni zaidi ya mwaka mmoja hawajapatiwa umeme; ni lini wananchi hao watapatiwa umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum Kagera, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkandarasi anayepeleka umeme katika Mkoa wa Kagera anaitwa JV Pomina Kwihaya, na yuko kazini anaendelea. Ni kweli alisuasua, katika wale wakandarasi saba ambao tulikuwa tunaona progress zao siyo nzuri na yeye alikuwemo. Lakini tumeweka strategy mpya na ninaamini Waheshimiwa Wabunge wengi wameona tumaenzisha ma-group ya whatsApp kwa ajili ya kupata updates za kila siku.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kabla ya mwaka huu kuisha umeme utakuwa umefika katika maeneo hayo kwa sababu ndiyo makubaliano yetu sisi na wakandarasi wote wanaopeleka umeme katika maeneo ya vijijini.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. halmashauri ya Kyerwa inawatumishi wa kada ya afya 252 ikiwa na mahitaji ya watumishi 1022 ni upungufu wa asilimia 75.

Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha kwenye hii halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa
Spika, katika ajira hizi ambazo Serikali imetangaza tutahakikisha pia na Halmashauri ya Kyerwa ina pata watumishi wa kwenda kwenye kada ya elimu na kada ya afya vile vile.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mpaka sasa barabara za vumbi ni zaidi ya asilimia 70 na barabara ya lami ikiwa ni asilimia 0.4 na changarawe asilimia 29.

Swali la kwanza, ni kwa nini bajeti imeendelea kuwa kidogo, ambayo ni shilingi bilioni tatu, wakati barabara za vumbi na za udongo bado ni zaidi ya asilimia 70?

Swali la pili, ni lini itatengenezwa barabara ya kutoka Kyerwa kwenda STAMICO ambako kuna biashara kubwa ya madini ya bati, ni lini barabara itatengenezwa, sambamba na kuunganisha Kata ya Mabira na Kata ya Kibale?

Mheshimiwa Spika, naomba majibu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa maelezo katika majibu yangu ya msingi, bajeti imeendelea kuongezeka ndani ya miaka hii mitatu. Ukiangalia trend mwaka wa fedha 2020/2021 bajeti katika Wilaya ya Kyerwa ilikuwa shilingi bilioni 1.26 tu, lakini hivi tunavyozungumza bajeti hiyo imekwenda mpaka shilingi bilioni 3.18 kwa maana imeongezeka mara mbili ya vile ilivyokuwa 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuiboreshea nchi yetu barabara zake za vijijini na mijini kupitia Wakala wa Barabara (TARURA). Kwa hiyo, nikutoea mashaka Mheshimiwa Mbunge, tutaendelea kuweka fedha kuangalia ni namna gani barabara hizi zinatengenezwa.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la barabara hii ya Kyerwa – STAMICO kupitia Kata ya Mabira na kadhalika, tayari katika kiwango cha lami tulianza kwa kujenga kilometa mbili kwenye Mji Mdogo wa Nkwenda, kuna barabara ambayo ipo kutoka Kido Hospitali katika Mji wa Kyerwa, vilevile tutakwenda sasa kuangalia hii kwenye bajeti zijazo tuweze kutenga fedha kwa ajili ya barabara hii ya Kyerwa mpaka STAMICO.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Barabara ya Bugene, Nkwenda mpaka Isingiro inasababisha ajali kwa sababu ya vumbi kubwa; Je, ni lini ujenzi wake utaanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante; labda tu cha kwanza ni kuhakikisha kwamba kama kuna vumbi ndiyo barabara zilivyo za vumbi, lakini Serikali imeendelea kutafuta fedha kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Pakiwa ni barabara ya vumbi haiepukiki, lakini Serikali inaendelea kutafuta fedha kuzijenga hizo barabara kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na kupunguza ajali kwenye maeneo husika. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Wananchi wa Kijiji cha Nyabikurungo Kata ya Ukuraijo waliwekewa nguzo na baadaye zikaondolewa bila kuunganishiwa umeme lakini pia Kijiji cha Bugaza, Kata ya Kimuli. Nataka kujua ni lini hawa wananchi watawashiwa umeme katika hayo maeneo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba programu yetu ya kupeleka umeme vijijini itakamilika mwezi Disemba mwaka huu. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kijiji hicho pia kitapata hiyo nishati ya umeme na mkandarasi anayepeleka umeme wa Rukomi na Kawahya tutamsimamia ili aweze kufanya kazi hiyo kwenye maeneo hayo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nataka kujua wananchi wa Kata ya Kamoli hutembea muda mrefu kufata chanzo cha Kitagata ambacho hakijatengenezwa vizuri, hivyo kukanyaga maji na kuchota maji machafu. Nataka nijue mkakati uliopo kuimarisha hicho chanzo cha maji lakini yakivutwa ili kuwa karibu na makazi ya watu badada ya kutembea umbali mrefu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata hii ya Kamoli kuboresha chanzo na kuleta usambazaji. Katika mwaka huu wa fedha Mheshimiwa Mbunge kuna kazi itafanyika kuona kwamba chanzo hiki kinaendelea kuwa toshelevu kinakuwa endelevu na usambazaji wa kuwasogezea huduma wananchi ni moja ya kazi yetu mama Wizara ya Maji, tutafanya hilo Mheshimiwa Mbunge.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wananchi wa Kata za Kimuli, Businde na Bugara hupata changamoto sana ya maji hasa tunapoelekea wakati huu wa kiangazi, lakini ni eneo ambalo lina mvua za kutosha: Je, ni nini mkakati wa Serikali wa kujenga matanki makubwa ili wakati wa mvua tuwe tunavuna maji na wakati wa kiangazi kama hiki tunachokiendea wananchi wanaweza kupata maji ili kuondoa adha wanayopitia kuchota maji ambayo ni tope? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kata hizi alizozitaja zina changamoto ya maji na sisi kama Wizara tunafahamu. Ushauri wa kujenga matanki makubwa tunauchukua, lakini vile vile tumejipanga kuhakikisha maeneo haya yote tunakwenda kuyapatia majisafi na salama. (Makofi)

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, ningependa kujua ni lini Serikali itajenga minara katika maeneo ya Mkoa wa Kagera ambayo ni pori la Kimisi lakini pia Pori la Biharamulo, ni mapori hatarishi na wakati mwingine mtu akipata ajali au..

SPIKA: Unatoa mchango Mheshimiwa?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, sawa, naomba kujua ni ni lini maeneo haya hatarishi yatawekewa mawasiliano kwa ajili ya kuokoa maisha ya watu.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANONA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kati ya mikoa ambayo imepata minara mingi sana katika minara 758 ni Mkoa wa Kagera, lakini kwa sababu Mheshimiwa Mbunge ameonyesha changamoto iliyopo katika maeneo ya mabonde, mapori pamoja na maeneo mengine, tutatuma timu yetu ya wataalam wetu, wataenda kujiridhisha na ukubwa wa changamoto hizo ili tujue hatua gani tutachukua kutatua changamoto hiyo, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ni suala la kawaida kuona sehemu “A” ina mtandao mmoja na sehemu “B” haina mtandao mwingine kwa maana hapa kuna Tigo, hapa kuna Vodacom.

Sasa ningetaka kujua ni utafiti gani ambao umefanyika na kuonesha mnara mmoja hauwezi kutoa mawasiliano ya mtandao zaidi ya mmoja? Moja, tukifanikisha hilo tutaweza kupunguza gharama, lakini pia tutaweza kupunguza madhara yanayotokana na hiyo mitandao au minara kwenye maeneo ya watu.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Kagera kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nitakuwa nimemuelewa vizuri anaongelea co–location; kama anaongelea co-location tunafanya cost benefit analysis ya watoa huduma anapoona kwamba hapa atakwenda kupata faida na pale atakapoona kwamba hawezi kupata faida hatoweza kufika pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana sasa Bunge lako tukufu lilipitisha Sheria Na. 11 ya mwaka 2006 kwa kuanzisha Mfuko wa Mawasiliano kwa wote ili kuhakikisha kwamba Serikali inakwenda kutoa ruzuku na kufikisha huduma ya mawasiliano katika maeneo ambayo hayana mvuto wa kibishara ili Watanzania wote wapate huduma ya mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa upande mwingine napokea ushauri wake na sisi tutaendelea kufanya utafiti ili kuboresha zaidi huduma ya mawasiliano nchini.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mkoa wa Kagera anaosema unachangia 2.6% ni mkoa ambao una rutuba ya kutosha, unazalisha kahawa ya kutosha na pia una ardhi ya kutosha: Je, huo mkoa kuchangia kwenye pato la Taifa 2.6% haioni kwamba ni kushindwa kwa Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Mkoa wa Kagera umezungukwa na nchi mbalimbali ikiwepo Rwanda, Burundi na maeneo mengine: Nini mkakati wa kuusaidia au kusaidia kuvutia wawekezaji katika huu mkoa ili uweze kuzalisha vya kutosha na hasa katika viwanda ili uongeze pato la Taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali haijashindwa na ushahidi wa hilo, Serikali imeweka mazingira wezeshi ili wananchi wenyewe wafanye shughuli zao za kiuchumi na kijamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, Serikali imefanya mikakati mbalimbali na hatua mbalimbali. Hivi leo tunaona sekta za uzalishaji ndiyo ambapo Serikali imeweka nguvu zaidi ya kuwekeza mfano kama kilimo cha umwagiliaji, mifugo na uvuvi, ahsante. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa kuwa watu wenye ulemavu kwanza kwa idadi siyo wengi, lakini wengi wao hupata changamoto hata ya kuwa na kipato: Ni kwa nini kusiwepo na tamko dhahiri kwamba kila mwenye ulemavu at least unaoonekana aweze kuvuka bure kwenye vivuko ili kuwapunguzia adha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, nimesema watu wenye ulemavu wanatofautiana kwa kiasi kikubwa sana, na wapo watu wenye ulemavu ambao wana uwezo pengine kukuzidi hata wewe Mheshimiwa Mbunge. Sasa ukisema tu mtu mwenye ulemavu yeyote asilipe, nadhani pia tutakuwa hatuwatendei haki. Tumesema watu wenye ulemavu ambao kweli vyombo vinaweza vikatambua huyu hana uwezo kwa kweli, hao wanatakiwa wasaidiwe, ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, wakati Serikali ikitumia gharama kutafuta vyanzo vya maji, Kyerwa ina vyanzo ambavyo viko tayari; moja ni Mto Kagera lakini na Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza, ni lini Ziwa Victoria na Mto Kagera vitatumika kuwapatia wananchi maji safi na salama ili itimie asilimia 80 kama maeneo mengine?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, wakati Serikali ikiwa na kaulimbiu ya kumtua mama ndoo hata miradi michache iliyopo ya maji wananchi hutembea umbali mrefu kwenda kufuata vyanzo hivyo vya maji.

Swali langu, ni lini au ni upi mkakati wa Serikali kuhakikisha maji hayo yanapatikana kwenye kaya za watu kama ilivyo maeneo ya mjini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Theonest kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, lini Serikali itatumia Ziwa Victoria? Kwenye bajeti yetu ya mwaka 2023/2024 Mheshimiwa Waziri alisisitiza hapa kwamba Ziwa Victoria ni moja ya chanzo ambacho kitaendelea kutumika kwa sababu tayari tumeanza kukitumia kwa maeneo ya Kyerwa na Kyerwa ni Jimbo ambalo nimekwenda mara tatu mimi mwenyewe na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo, kwa hiyo, ni jimbo ambalo nimelifanyia kazi sana. Lengo ni kuhakikisha kwamba kwenye hili swali lako la pili kwamba lini kuona kwamba maeneo yote yatafanyiwa kazi kupata maji safi? Ndio kazi inayoendelea na ni maagizo ya Mheshimiwa Makamu wa Rais ambaye nilikwenda naye pale Kyerwa lakini na sisi kama Wizara tunaendelea kuyafanyia kazi Jimbo la Kyerwa.
MHE. ANATROPIA L. THEOENEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; barabara ya Benako kuja Karagwe haina lami na hii ni barabara muhimu sana kwa sababu ya ulinzi, kule kuna utekajeji lakini pia ufanyaji wa biashara kati ya Tanzania na Rwanda. Swali ni lini hiyo barabara itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ambayo inaanzia Bugene kupitia Chato hadi Benako ni barabara ambayo inaunganisha pia na nchi yetu Uganda nchi yetu, lakini pia kwenda Rwanda. Barabara hii ipo mbioni kuanza kujengwa kilometa 62 kwa kiwango cha lami na ipo kwenye mpango kuanzia mwaka huu wa bajeti. Ahsante. (Makofi)

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri amenijibu mchakato. Najua na ninatambua taratibu kwamba lazima hiyo michakato ifanyike. Sasa swali langu linabaki, ni lini? Kwa sababu natambua mtatangaza zabuni na Serikali inafuata utaratibu na schedule; kwa hiyo, nataka kujua ni lini? Hilo ni swali la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Wilaya ya Kyerwa, TANROADS ina mtandao mdogo wa barabara ya Kyerwa na TARURA wana mzigo mkubwa ikiwepo na madaraja: Je, Serikali haioni ni wakati muhimu wa kutanua mtandao wa barabara kuunganisha Kata ya Nkwenda - Songambele pamoja na Karagwe na Rwanda kwa upande wa Kusini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY KASEKENYA MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, huu tena siyo mchakato, tumetaja tarehe 10 mwezi huu wa Tano, zabuni imefunguliwa. Ukishafungua zabuni, maana yake tayari unaanza kujenga utakapokuwa umempitisha Mkandarasi baada ya kufanya evaluation.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, zipo taratibu ambazo zinafuatwa ili barabara zipandishwe kutoka hadhi ya kuhudumiwa na TARURA na kuhudumiwa na TANROADS. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba viko vikao ambavyo vinapitia, zinaletwa kwenye Wizara, Wizara inaenda kufanya tathmini na kuona hizi barabara zinakidhi vigezo halafu zinapandishwa kutoka TARURA kuja TANROADS? Ahsante. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; Tarafa ya Murongo imepatakana na Mto Kagera ambako ni chanzo kikubwa cha maji, lakini hizo kata hazina maji.

Nataka kujua nini mkakati wa Serikali katika kuwatua kina mama ndoo kusaidia upatikanaji Kata ya Kibingo, Bugomora, Murongo, Kibale, Kimuli, Bugara na Businde? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tarafa hiyo ya Murongo aliyoitajwa ni moja ya maeneo tunaendelea kuyafanyikazi na kwasababu ipo karibu na chanzo cha uhakika naomba nitoe wito kwa wananchi tuendelee kuvumilia, tunakotoka ni mbali tunakokwenda ni karibu, hizi kata zote zinakwenda kupata huduma ya maji na salama.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Wilaya ya Kyerwa ina vijiji 29 ambavyo bado havijapatiwa umeme ikiwemo Kata ya Nkwenda Kijiji cha Kakerere, Kata ya Kakanja Kijiji cha Keshanda na Kata ya Lukolaijo Kijiji cha Mgorogoro. Navitaja hivi kwa sababu vipo mjini. Ni lini hivyo vijiji vitapatiwa umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni committment na Serikali kwamba itakapofika Desemba mwaka huu vijiji vyote viwe vimepelekewa umeme mabadiliko na nyongeza kidogo itatokana na changamoto ambazo wakati tunawasilisha bajeti tulizisema. Ila Kyerwa ni eneo mojawapo ambalo mkandarasi yupo site na kazi zinaendelea na tunaamini kwamba kazi itakamilika kwa jinsi tulivyojipangia. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Halmashauri ya Kyerwa ni moja kati ya Wilaya mpya ambayo pia haina Kituo cha Polisi, hivyo OCD utumie ofisi ndogo ambayo iko Kagenyi, wananchi tayari wameanza tayari ujenzi wa kituo cha polisi cha wilaya.

Nataka nijue ni lini Serikali itawapelekea fedha ili waweze kumalizia ujenzi ambao wameuanzisha kwa nguvu zao wenyewe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: - (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tunatambua uwepo wa halmashauri au wilaya nyingi ambazo hazina vituo vya polisi vya Wilaya kwa maana ya OCDs officce na niwashukuru halmashauri ambazo wanatoa majengo kwa ajili ya kutumiwa na wenzetu wa polisi ni muahidi tu Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo nimekuwa nikisema katika majibu ya nyongeza hapa, ya maswali ya msingi tunaendelea kujenga vituo vya polisi kwenye mikoa na wilaya ambazo hazina kabisa vituo hivyo. Kwa hiyo, Wilaya ya Kyerwa ni moja ya wilaya ya kipaumbele hasa ukizingatia kwamba iko mpakani pale ambapo itatokea tutapata fedha tutaipa kipaumbele cha juu. Nashukuru. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Mji wa Nkwenda ni moja kati ya miji ambayo iliahidiwa kujengewa kilometa tano za lami, hata hivyo kilometa tano hazikujengwa ndani ya mji zilijengwa katika barabara ya TANROADS ambayo inapita nje ya mji.

Sasa nataka kujua ni lini kilometa tano zilizoahidiwa kujengwa katika barabara za ndani ya Mji wa Nkwenda zitajengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua ahadi za viongozi hususan katika maeneo yote ikiwemo eneo la Kwera ambalo umeliainisha hapa Nkwenda na kwa hili ambalo amelieleza ni kwamba Serikali itaendelea kutekeleza kadri ambavyo tutapata fedha, ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Kutokana na majibu aliyonipatia ni wastani wa wanawake 24 huwaguliwa kila baada ya Uchaguzi Mkuu. Kwa hiyo, naona kwamba ongezeko ni dogo wanawake 24 kila baada ya miaka mitano ni wachache sana kuwakulisha licha ya Serikali kuridhia mikataba mbalimbali ya kimataifa kuongeza ushiriki wa wanawake. Swali langu ni mkakati gani mahususi unaopaswa kuwa revised ili kuongeza idadi ya wanawake kwenye siasa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Mkakati gani wa Serikali wa kubadilisha Political Parties Act ili kuweka kifungu kitakachovilazimisha vyama vya siasa kuwa na idadi maalumu ya wanawake watakaokuwa wagombea kwenye chaguzi mbalimbali kwenye hii nchi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Kwanza nisema Serikali inatambua na kuthamini sana sana ushiriki wa wanawake katika shughuli za kisiasa na lakini na maeneo mengine. Niseme tu katika eneo hili mkakati uliopo ndani ya msajili wa vyama vya siasa ni kuendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali ya wanawake kuendelea kujiamini na waweze kujiandaa kugombea nafasi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namba mbili, tutaleta Bungeni mabadiliko ya Sheria ya vyama vya siasa ili kuvitaka vyama sasa kuwa na Sera ambayo itaweka mwongozo mahususi wa kujumuisha wanawake kwenye kugombea nafasi mbalimbali. Kwa hiyo, niwaondoe shaka wanawake wenzangu Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anawajali anawathamini na tutaendelea kufanya vizuri kwenye eneo hili la kuhakikisha tunawajumuisha wanawake kwenye ngazi zote za maamuzi, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Licha ya mkakati wa Serikali kuruhusu minada ya kahawa, Mkoani Kagera, bado changamoto ya bei inabaki kuwa chini ukilinganisha za majirani zetu wa Uganda, hivyo kupelekea watu kutamani kuvusha kahawa. Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha bei ya kahawa Mkoani Kagera haitofautiani sana na Uganda ili watu waweze kupata faida ya kahawa zao?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Swali la namna hii nilijibu nafikiri ndani ya siku mbili au tatu zilizopita, tukaainisha moja ya mchakato wa Serikali wa kuongeza thamani katika zao la kahawa ambao utachangia ongezeko la bei kwa sababu asilimia kubwa ya kahawa ambayo tunauza sisi ni kahawa ghafi ambayo inapelekea bei kuwa chini. Nimthibitishie kwamba mkakati wetu juu ya uwekezaji katika zao la kahawa uko palepale na tutawasaidia wakulima katika maeneo yote nchini wanayolima ikiwemo katika Mkoa wa Kagera. Kwa hiyo nimwondoe shaka Mbunge katika hili, hii kazi tunaiweza na tutaifanya. Ahsante.