Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Anatropia Lwehikila Theonest (26 total)

MHE. SOPHIA M. SIMBA (K.n.y. MHE. ANATROPIA L. THEONEST) aliuliza:-
Kuna mgogoro wa ardhi baina ya wananchi wa Kipunguni „A‟ na Kipunguni Mashariki dhidi ya Mamlaka ya Uwanja wa Ndege Jijini Dar es Salaam. Wananchi hao wanapinga uthamini uliofanywa na fidia kidogo kwa kikundi cha watu wachache, huku wengine wakizuiwa kuendeleza maeneo yao?
(a) Je, ni lini Serikali itaenda kumaliza mgogoro huo uliodumu tangu 2007?
(b) Je, Serikali ipo tayari kuwapa fidia ya kiwango cha soko wananchi waliozuiwa kuendeleza maeneo yao na kuendelea kubaki maskini kwa muda wote huo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali Na. 417 la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Kipunguni “A” na Kipunguni Mashariki pamoja na maeneo ya Kipawa pamoja na Kigilagila ni maeneo yaliyotwaliwa na Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege mwaka 1997. Uthamini wa maeneo haya ulifanywa na Kampuni ya Tanvaluers and Property Development ambayo ni kampuni binafsi ya uthamini na ilifanya mwaka 1997. Hata hivyo, malipo ya fidia hayakuweza kufanyika kwa wakati. Mwaka 2011 Serikali iliamua kuanza kuwalipa wananchi hao fidia kwa kuanza na eneo la Kipawa na Kigilagila.
Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kuwa Sheria iliyotumika kufanya uthamini huo ilikuwa ni ile ya Utwaaji Ardhi ya mwaka 1967 yaani (The Land Acquisition Act of 1967) ambayo ilipwaji wa fidia ulipaswa kuzingatia yafuatayo:-
(i) Maendelezo pekee (yaani majengo na mazao katika eneo);
(ii) Kiwanja mbadala; na
(iii) Riba ya 6% kwa kila mwaka pindi malipo yanapocheleweshwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 2010 wananchi hao walifungua kesi Mahakama Kuu wakipinga kulipwa fidia kwa kutumia sheria ya zamani, wananchi walishindwa kesi hiyo, kwani mchakato wa utwaaji wa eneo hilo ulianza ndani ya Sheria ya zamani ya Utwaaji Ardhi na sio Sheria mpya ya mwaka 1999 ambayo ilianza kutumika mwaka 2001. Sheria hii mpya inataka malipo ya fidia yalipwe kwa kuzingatia yafutayo:-
(i) Thamani ya ardhi;
(ii) Thamani ya maendelezo;
(iii) Posho za makazi, usumbufu na usafiri; na
(iv) Riba ya kiwango cha soko pale malipo yanapocheleweshwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hukumu hiyo stahili ya wananchi hao ni fidia ya maendelezo, viwanja mbadala na riba ya 6% kwa mwaka mpaka pale malipo yatakapofanyika kama ilivyobainishwa katika Sheria ya Utwaaji Ardhi ya mwaka 1967. Mnamo mwaka 2011 wananchi wa maeneo ya Kipawa na Kigilagila walilipwa fidia yenye wastani wa shilingi bilioni 18. Wananchi wa eneo la Kipunguni bado hawajalipwa fidia zao. Serikali kupitia mamlaka ya viwanja vya ndege ipo katika mkakati wa kutafuta fedha hizo ili kuwalipa wananchi stahiki zao.
MHE. PAULINE P. GEKUL (K.n.y. MHE. ANATROPIA L.
THEONEST aliluiza:-
Mkao Makuu ya Wilaya ya Kyerwa yamewekwa katika Kata ya Kyerwa.
Je, ni mchakato gani ulifanyika mpaka Kata ya Kyerwa kuwa Makao Makuu ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA
SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili eneo liwe na makao makuu ya Wilaya lazima wananchi washirikishwe kupitia mikutano mikuu ya Vijiji na Halmashauri za Vijiji, Kamati za Maendeleo za Kata, Mabaraza ya Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Kamati ya Ushauri ya Mikoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uamuzi wa kuifanya Kata ya Kyerwa kuwa Makao Makuu ya Wilaya ya Kyerwa ulitolewa baada ya kupitishwa na Baraza la Madiwani katika kikao cha tarehe 30 hadi 31 Oktoba, 2012 na Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Kagera katika kikao chake cha tarehe 15 Machi, 2013 hivyo uamuzi wa mwisho kuhusu eneo la Rubwera katika Kata ya Kyerwa kuwa Makao Makuu ya Wilaya Kyerwa ulizingatia mapendekezo ya vikao hivyo vya kisheria.
MHE. MWITA M. WAITARA (K.n.y. MHE. ANATROPIA L. THEONEST) aliuliza:-
Kuna mgogoro wa ardhi baina ya wananchi wa Kipunguni ‘A’ na Kipunguni Mashariki dhidi ya Mamlaka ya Uwanja wa Ndege Jijini Dar es Salaam. Wananchi hao wanapinga uthamini uliofanywa na fidia kidogo kwa kikundi cha watu wachache huku wengine wakizuiwa kuendeleza maeneo yao.
(a) Je, ni lini Serikali itaenda kumaliza mgogoro huo uliodumu tangu mwaka 2007?
(b) Je, Serikali ipo tayari kuwapa fidia ya kiwango cha soko wananchi waliozuiwa kuendeleza maeneo yao na kuendelea kubaki maskini kwa muda wote huo?
NAIBU WAZIRI WA WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, aah samahani naona Mzee Waitara ameniroga hapa.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a ) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali ilifanya uthamini wa ardhi katika maeneo ya Kipunguni ‘A’ na Kipunguni Mashariki ikiwa ni pamoja na maeneo ya Kigilagila na Kipawa mwaka 1997 kwa kuwashirikisha wakazi wa maeneo husika kwa mujibu wa Sheria ya Utwaaji Ardhi (Land Acquisition Act) ya mwaka 1967 ambayo inaainisha mambo ya kuzingatia ikiwa ni thamani ya mazao na majengo yaliyopo kwenye maeneo husika, kumpatia mkazi wa eneo linalotwaliwa kiwanja na vilevile kulipa riba ya asilimia sita kwa mwaka pale ambapo malipo yanacheleweshwa.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali haikuwa na fedha za kutosha kuwalipa wakazi wote kwa pamoja, malipo yalifanyika kwa awamu tatu kadri fedha zilivyokuwa zinapatikana. Awamu ya kwanza na ya pili ya mwaka 2009 - 2011 ilihusu malipo ya wakazi wa Kipawa na Kigilagila na katika awamu ya tatu ambayo ilitolewa mwaka 2014 ililipa baadhi ya wakazi wa Kipunguni ambao idadi yao ilikuwa 59.
Mheshimiwa Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, kwa sasa Serikali imekusudia kumaliza kulipa fidia wananchi waliobaki katika maeneo hayo kwa bajeti ya mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kwamba viwango vya ulipaji fidia huzingatia sheria iliyotumika kufanya uthamini husika. Hivyo kwa kuwa uthamini wa maeneo ya Kipunguni ‘A’ na Kipunguni Mashariki ulifanyika mwaka 1997 kwa mujibu wa Sheria ya Utwaaji Ardhi ya mwaka 1967 malipo au fidia kwa wakazi wa maeneo husika yatazingatia matakwa ya sheria hiyo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-
Jimbo la Segerea ni moja kati ya Majimbo ya Dar es Salaam ambalo wakazi wake ni wengi na wa kipato cha chini na sababu kubwa ikiwa ni ubovu wa miundombinu ya barabara hasa madaraja na mitaro, hivyo kusababisha mafuriko ya mara kwa mara.
Je, ni lini Serikali itajenga madaraja ya Tabata Kisiwani na Kisukuru sambamba na kujenga mitaro ili kupunguza adha ya mafuriko katika Kata za Jimbo hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuhudumia wananchi wa Jimbo la Segerea katika kuboresha na kufanya matengenezo ya miundombinu ya barabara, madaraja pamoja na mitaro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutatua tatizo la adha ya mafuriko yanayotokana na mvua maeneo ya Tabata, Halmshauri ya Manispaa ya Ilala kupitia mradi wa DMDP imepanga kujenga mifereji ya maji ya mvua yenye urefu wa kilometa 9.82 na vivuko katika bonde la Msimbazi – Tenge – Lwiti – Sungura na Tembomgwaza kwa gharama ya shilingi bilioni 15 ambazo zabuni za ujenzi huo zinatangazwa mwezi Mei, 2018. Hivyo, baada ya ujenzi wa mifereji hiyo na vivuko, tatizo la mafuriko kwa wananchi wa Tabata Kisiwani na Kisukuru litapungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mawenzi - Tabata - Kisiwani kwa mwaka wa fedha 2016/2017 ilitengewa shilingi milioni 180 za kufanyia matengenezo kwa kiwango cha Changarawe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Manispaa ya Ilala imeyenga shilingi milioni 40 za kuifanyia matengenezo ya kawaida na kukarabati daraja lililopo eneo la Mwananchi.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-
Jimbo la Segerea ni kati ya majimbo yaliyosahaulika katika miundombinu ya barabara na kupelekea mitaa mingi kuwa na madimbwi sugu na mafuriko kila mvua inaponyesha. Kadhia hii imepelekea barabara za mitaa kupitika kwa taabu na kupelekea foleni kubwa katika barabara ya Segerea mpaka barabara ya Mandela kwa kuwa ndiyo barabara pekee inayotumiwa na wananchi.
Je, ni lini jimbo hili litatengewa bajeti kwa barabara zake za mitaa kwa kiwango cha lami, changarawe na ujenzi wa mifereji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya barabara inayoendelea kutekelezwa kwa kiwango cha lami sambamba na mifereji katika Jimbo la Segerea ina thamani ya shilingi bilioni 4.6 ambapo Halmashauri ya Manispaa ya Ilala imetoa shilingi bilioni 2.6 na shilingi bilioni 2.0 zimetolewa na Mfuko wa Barabara. Miradi ya barabara inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na barabara za Mnyamani kilometa 2.3 kwa shilingi bilioni 2.5; Tabata Barakuda – Chang’ombe kilometa 0.5 kwa shilingi milioni 744 na Tabata – Kimanga – Mazda kilometa 0.8 kwa shilingi bilioni 1.4.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Jimbo la Segerea limetengewa shilingi milioni 880 ambapo kati ya fedha hizo shilingi milioni 380 zitatengeneza kwa kiwango cha changarawe barabara za Bonyokwa – Kisukuru- Majichumvi; Tabata – Mawenzi – Kisiwani; Chang’ombe – Majichumvi; Chang’ombe - Mbuyuni, Guest Nyekundu – Jumba la Dhahabu na shilingi milioni 500 zitatumika kufanya usanifu na ujenzi wa madaraja ya Mongolandege na Nyebulu.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-
Nkwenda I ni kata ya kibiashara yenye wakazi wengi, na Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, wakati wa kampeni katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 aliahidi kujenga barabara kwa kiwango cha lami.
Je, Serikali haioni ni wakati muafaka kujenga kilometa kadhaa za lami ili kupunguza adha wanazopata wafanyabiashara hao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, aliahidi kujenga barabara yenye urefu wa kilometa tano katika Wilaya ya Kyerwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jitihada za kutekeleza ahadi hii zimekwishaanza na katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) imetenga shilingi milioni mia tatu hamsini kwa ajili ya ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa moja kwa kiwango cha lami Makao Makuu ya Wilaya ya Kyerwa (Rubwera). Ujenzi huu unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2018. Serikali itaendelea kujenga barabara za lami Wilaya ya Kyerwa kwa awamu ili kutimiza ahadi hiyo ya Mheshimiwa Rais.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua Jengo la Mama na Mtoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ambalo hata akinamama wajawazito wawili hawawezi kupishana kwenye corridor?

(b) Je, Serikali haioni kuwa kupanua eneo la jengo hilo kutaenda sambamba na kuhamasisha wanaume kwenda kliniki na wenza wao na kupata ushauri pamoja?

(c) Katika eneo la kujifungulia la akinamama ni rahisi kuona kitanda cha jirani yako; je, Serikali haioni hali hii ni udhalilishaji pamoja na kuingilia uhuru wa mwingine kujihifadhi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa lengo la kuboresha huduma za akinamama wajawazito, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, mnamo mwaka 2016 alielekeza kuwa Ofisi za Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamiii, Jinsia, Wazee na Watoto zilizokuwa eneo la Hospitali ya Taifa Muhimbili kuhama na jengo hilo kutolewa kwa Hospitali ya Taifa ili kupunguza msongamano wa akinamama wajawazito katika jengo la Maternity I. Hivyo basi, ikumbukwe kuwa jengo hili lilikuwa ni Ofisi na lilibadilishwa matumizi kuwa jengo la mama na mtoto, hivyo, miundombinu ya jengo hili hairuhusu kufanyiwa upanuzi.

Mheshimiwa Spika, jengo hili limewekwa viti vya kutosha katika corridor ambayo vinatosheleza kukaa akinamama pamoja na wenza wao. Natoa rai kwa wanaume kuambatana na wenza wao kliniki ili kupata elimu ya kutunza ujauzito; maandalizi ya kujifungua na matunzo ya mtoto ajaye, mwitikio kwa sasa kwa wanaume sio wa kuridhisha.

Mheshimiwa, Spika huduma za akinamama hasa za kujifungua zinahitaji usiri mkubwa. Hiki ni kipaumbele cha Serikali na kwa Watumishi wa Afya katika vituo mbalimbali nchini. Hivyo, katika jengo hili eneo la kujifungulia lina vitanda 20 ambavyo vimetenganishwa na mapazia imara (screen folds) ambapo akinamama hawaonani wakati wa kujifungua na hivyo kutunza faragha zao.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, ni lini barabara ya Segerea – Sheli kwenda Kipawa kupitia Seminari itaanza kutengenezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Segerea – Sheli – Kipawa kupitia seminari yenye urefu wa kilometa 2.93 inasimamiwa na TARURA Manispaa ya Ilala, imesajiliwa kwa jina la Majumba Sita, Sitakishari. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, barabara hiyo imechongwa kwa grader ili kuiwezesha kupitika. Hata hivyo, barabara hii inakatisha katika mto Msimbazi ambapo hakuna daraja. Daraja linalohitajika kujengwa ni kubwa na usanifu wake ulishafanyika.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo inatokana na mto kutanuka, hivyo inahitajika kufanyiwa study ya kina na mapitio ya usanifu wa awali ili kupata mahitaji halisi ya ujenzi wa daraja kutokana na changamoto hiyo. Mara baada ya kukamilika kwa mapitio ya usanifu na tathmini ya gharama Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kujenga daraja na kuifanyia matengenezo makubwa barabara hii. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali kupitia TARURA imeitengea barabara hii jumla ya shilingi milioni 43 kwa ajili ya matengenezo ya maeneo korofi.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalipa fidia wananchi ambao maeneo yao yalichukuliwa kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Uwekezaji vya Nkwenda na Murongo?

(b) Je, ni lini ujenzi wa Vituo hivyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge kuwa ujenzi unaotarajiwa kufanyika ni wa Masoko ya Kimkakati ya Kimataifa ya Nkwenda na Murongo na sio Vituo vya Uwekezaji kama alivyouliza swali lake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inamiliki maeneo yanapojengwa masoko ya Kimkakati ya Nkwenda na Murongo kwa asilimia 100. Eneo la kiwanja cha soko la kimkakati la Nkwenda lilikuwa chini ya Serikali ya Kijiji cha Nkwenda na lilitumika kama shamba kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Kijiji (MFUMAKI). Eneo hilo liliendelea kutumika kama shamba darasa (Farmers Extension Centre Demonstration Area) chini ya Wizara ya Kilimo, hivyo halihitaji fidia. Aidha, Eneo linapojengwa soko la kimkakati la Murongo ni mpakani mwa Nchi ya Tanzania na Uganda linalomilikiwa na Serikali, hivyo halihitaji fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Masoko ya Kimkakati ya Kimataifa ya Nkwenda na Murongo ni masoko yaliyokuwa yanajengwa kama sehemu ya utekelezaji wa Programu ya kuendeleza Sekta ya Kilimo (Agricultural Sector Development Program-ASDP) kupitia Mradi wa Uwekezaji katika sekta ya kilimo ngazi ya Wilaya (District Agricultural Sector Investment Project- DASIP). Ujenzi wa masoko hayo mpaka sasa umekamilika kwa asilimia hamsini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Kilimo inayoratibu Programu ya kuendeleza Sekta ya Kilimo katika bajeti ya mwaka wa fedha 2019/2020, imetenga shilingi bilioni 2.5 fedha za ndani kwa ajili ya kukamilisha mradi wa ujenzi wa masoko ya kimkakati. Katika kuhakikisha kuwa ujenzi wa masoko hayo unakamilika na kuanza kutumika, Wizara ya Kilimo imetuma wataalam kutoka Wakala wa Nyumba (TBA) kwa ajili ya kufanya tathmini ya gharama za umaliziaji wa ujenzi wa masoko hayo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST Aliuliza:-

Je, Serikali imefikia wapi katika mchakato wa kulipa fidia kwa wananchi wa Kipunguni waliotakiwa kusitisha kuendeleza maeneo yao ili kupisha upanuzi wa kiwanja cha ndege?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (ELIAS J. KWANDIKWA) Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonist, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa wananchi 1,182 eneo la Kipunguni yaani wananchi 381 Kipunguni Mashariki na wananchi 801 Kipunguni A ambao maeneo yao yalifanyiwa uthamini kwa ajili ya kulipwa fidia baada ya maeneo hayo kuwekwa kwenye mpango wa kutwaliwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kufuatia mradi wa maboresho ya miundombinu na usalama wa Kiwanda cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam yanayoendelea kufanywa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi ambao maeneo yao yapo kwenye eneo la mradi kuwa Serikali itawalipa fidia pale itakapotenga fedha kwa ajili ya mradi husika.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, Megawati moja ya umeme inazalishwa kwa bei gani na inauzwa kwa bei gani (unit cost)?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA (K.n.y. WAZIRI WA NISHATI) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini, inagharamia uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme hadi kwa mteja kwa kuweka miundombinu husika ya umeme. Kwa sasa gharama ya kuzalisha uniti moja (Kwh) ya umeme kwa kutumia chanzo cha maji ni shilingi 36 na gharama ya kuzalisha uniti moja ya umeme kwa kutumia gesi asilia ni wastani wa shilingi 150. Gharama ya kuzalisha uniti moja kwa mitambo inayotumia mafuta ya dizeli katika maeneo yaliyopo nje ya Gridi ya Taifa ni shilingi 720 kwa uniti moja yaani Kwh moja.

Mheshimiwa Spika, bei ya kuuza umeme inatokana pia na gharama za kuzalisha, kusafirisha na kusambaza umeme. Kwa sasa bei ya kuuza umeme ni wastani wa shilingi 242 kwa uniti yaani Kwh.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST Aliuliza:-

Je, ni likizo ya muda gani wamekuwa wakipewa wazazi (watumishi wanawake na wanaume) pale wanapopata watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni H. 12(2) ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za Mwaka 2009, mtumishi wa umma mwanamke anapojifungua mtoto hupewa likizo ya uzazi ya muda wa siku 84 mara moja kila baada ya miaka mitatu. Hata hivyo, kwa mujibu wa Kanuni H. 12(3) ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009, mtumishi husika anapojifungua watoto zaidi ya mmoja hupewa siku 14 zaidi za likizo ya uzazi na hivyo kuweza kuwa siku 98. Kanuni tajwa haikubanisha muda wa likizo ya uzazi kwa mtumishi anayejifungua mtoto njiti.

Mheshimiwa Spika, matukio ya uzazi wa mapacha zaidi ya wawili (triple) na watoto njiti ni nadra kutokea mara kwa mara. Hivyo, Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009 hazikuainisha masharti ya likizo ya uzazi kwa matukio kama hayo. Hivyo, natoa wito kwa waajiiri na wasimamizi wa rasilimaliwatu katika utumishi wa umma kutoa taarifa kwa Katibu Mkuu wa Utumishi na kuomba kibali cha kuongezewa muda wa likizo ya uzazi kwa watumishi wa umma walio chini yao pindi wanapojifungua watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni H.13 ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009, Mtumishi wa Umma mwanaume hupewa likizo ya uzazi ya angalau siku tano kuanzia siku ya kuzaliwa mtoto ili aweze kuhudumia familia yake. Hata hivyo, iwapo kuna sababu za msingi zinazomlazimisha kuendelea kuhudumia familia kwa ukaribu, mtumishi husika anaweza kuomba ridhaa kwa mwajiri wake ya kuongezewa ili siku kadhaa kuhudumia familia.

Mheshimiwa Spika, hivyo, inapotokea mtumishi wa umma kajifungua watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti na kulazimika kuwa na muda wa zaidi wa kuhudumia watoto hao, mwajiri wake anapaswa kuwasilisha hoja kwa Katibu Mkuu (Utumishi) ilia toe kibali cha kuongeza muda wa likizo ya uzazi. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

(a) Je, ni kwa nini Serikali inawazuia wakulima wanaoshirikiana na sekta binafsi, kuuza mazao yao ya biashara hasa kahawa, mahindi na korosho nje ya nchi kwa lengo la kujipatia faida?

(b) Je, ni kwa nini Serikali isiongeze ruzuku ya NFRA ili inunue mazao hayo pindi bei zinaposhuka?
WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lweikila Theonest – Mbunge Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Kilimo imekuwa na inaendelea kutoa vibali kwa wakulima na wafanyabiashara mbalimbali wanaosafirisha mazao ya kilimo hususan mahindi nje ya nchi au kuingiza ndani ya nchi. Vibali vitolewavyo na Wizara ya Kilimo ni vya kuingiza mazao ya kilimo nchini au kusafirisha mazao ya kilimo nje ya nchi (Import and Export Permits) pamoja na cheti cha Usafi wa Mazao yanayosafirishwa (Phytosanitary Certificate).

Mheshimiwa Spika, Serikali haina mpango wa aina yoyote wa kuwazuia wakulima kushirikiana na sekta binafsi kuuza mazao yao nje ya nchi na Serikali inaendelea kuhimiza wakulima waendelee kujiunga katika vikundi ili waweze kuwa na nguvu ya pamoja katika kuuza mazao yao na kuweza kuongezea thamani mazao yao ili waweze kujiongezea kipato zaidi.

(b) Mheshimiwa Spika, Majukumu ya Wakala wa Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) ni kununua na kuweka akiba ya chakula cha Taifa, kudhibiti mfumuko wa bei wa vyakula vya nafaka kwa kuingiza nafaka sokoni ya bei nafuu pamoja na kutoa chakula cha msaada kwa maelekezo ya Mfuko wa Maafa wa Taifa pindi Taifa linapopatwa na majanga ya maafa. Kwa kuzingatia majukumu hayo, Wakala umekuwa kimbilio la wakulima kwa kuwa umekuwa ukinunua nafaka kwa bei nzuri katika masoko inayozingatia gharama za uzalishaji za mkulima.

Mheshimiwa Spika, Serikali hutenga ruzuku kwa ajili ya ununuzi wa nafaka kila mwaka. Kwa kuzingatia majukumu ya Wakala, ununuzi huu hauhusishi mazao yasiyo ya nafaka. Aidha, Wakala hutumia vyanzo vingine vya mapato kununua nafaka zikiwemo mauzo ya nafaka na mikopo kutoka taasisi za fedha, mikopo ambayo hurejeshwa kwa kutumia fedha za mauzo ya nafaka.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST Aliuliza: -

Mfumo wa ununuzi wa kahawa kupitia Vyama vya Ushirika umekuwa mwiba kwa wananchi wa Kyerwa na Karagwe kupitia KDCU:-

(a) Je, kwa nini Serikali isiruhusu watu binafsi kununua kahawa moja kwa moja toka kwa mkulima?

(b) Je, ni lini wakulima wanaodai watalipwa fedha zao?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Anatropia kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wa ununuzi wa kahawa hapa nchini unawaruhusu wanunuzi binafsi kununua kahawa kutoka kwa wakulima kupitia Vyama vya Ushirika.

Kahawa inayoruhusiwa kwa wanunuzi binafsi ni ile ambayo tayari imepitia utayarishaji wa ngazi ya awali na ikiwa tayari kupelekwa kiwandani au kuuzwa kwenye soko la mnada au soko la moja kwa moja. Pia Vyama vya Ushirika vinaruhusiwa kuingia makubaliano na kampuni binafsi kupitia utaratibu wa kilimo cha mkataba, utaratibu wa wafanyabiashara kwenda moja kwa moja kwa wakulima, maarufu katika Mkoa wa Kagera butura, hauruhusiwi kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera hadi kufikia tarehe 20 Januari, 2021 katika msimu wa 21 jumla ya wanunuzi binafsi saba wamenunua kiasi cha kilo milioni 13 za kahawa maganda kupitia kwenye Vyama vya Ushirika. Kutokana na maboresho hayo ya kuruhusu wanunuzi binafsi na Vyama vya Ushirika wameweza kulipa bei ya Sh.1,200 kwa kilo ya kahawa ya maganda kwa msimu wa 21 ukilinganisha na kiasi cha Sh.1,100 kwa kilo katika msimu uliotangulia wa mwaka 2020. Aidha, Bodi ya Kahawa itatoa vibali mapema kwa wafanyabiashara binafsi ambao wako tayari kununua kahawa katika msimu wa mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, Chama Kikuu cha Ushirika cha Wilaya ya Karagwe (KDCU) katika msimu wa kahawa wa mwaka 2020/2021 kimekusanya kahawa maganda kilogramu milioni 40.5 zenye thamani ya shillingi bilioni 48 kutoka katika Vyama vya Msingi 123. Aidha, hadi kufikia tarehe 18 Januari, Chama Kikuu cha Ushirika (KDCU) kilishamaliza malipo yote ya wakulima wa Mkoa wa Kagera.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Pamoja na Kyerwa kuwa na wakulima wengi wa kahawa bado soko linakuwa gumu.

Je, ni lini Serikali itafikiria kubadilisha mfumo wa ununuzi wa kahawa kwa wakulima?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uzalishaji wa kahawa umeongezeka kutoka tani 47,000 kwa mwaka 2016/2017 mpaka tani 59,000 kwa mwaka 2019/2020. Aidha, katika msimu wa 2020/2021 lengo la uzalishaji ni tani 70,000 za kahawa safi, ambapo hadi kufikia Machi, 2021 uzalishaji umefikia tani 67,676 sawa na asilimia 96.7 ya lengo. Kati ya hizo, Mkoa wa Kagera pekee unazalisha tani 39,667 ambayo ni sawa na asilimia 58.8 ya uzalishaji wa nchi nzima na Wilaya ya Kyerwa inazalisha tani 19,000 kati ya 39,000 zinazozalishwa na Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Spika, katika msimu wa 2020/2021 mifumo ya masoko inayotumika ni soko la awali, mnada na soko la moja kwa moja. Katika mifumo yote, wakulima hukusanya kahawa yao kupitia vyama vya ushirika. Mifumo hiyo inalenga kuondoa biashara ya kahawa isiyo rasmi inayotumiwa na walanguzi maarufu kwa majina ya butura (Kagera), Njemke au kata kichwa kwenye mikoa mingine ikiwemo Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Mheshimiwa Spika, katika msimu wa 2020/2021 tani 67,676 zilizozalishwa tayari zimeuzwa kufikia Machi, 2021, tani 20,296 zenye thamani ya Dola za Kimarekani Milioni 53.5 sawa na asilimia 30 za mauzo yote zimeuzwa kwa njia ya mnada. Kadhalika, kufikia Machi mwaka huu jumla ya tani 47,108 zenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 79.2 sawa na asilimia 69.9 ya kahawa yote iliyouzwa zimeuzwa kwa njia ya minada.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa sasa inaamini mifumo ya masoko inayotumika ni mizuri na itaendelea kuboreshwa kulingana na mahitaji yanavyojitokeza ili kuhakikisha wakulima wanapata masoko ya uhakika na yanayotoa bei nzuri. Hatua zinazoendelea kuchukuliwa kwa sasa ni kuimarisha bei za kahawa kwa kuongeza ubora kuanzia shambani hadi sokoni, kuongeza tija ili wakulima waongeze kipato na kuimarisha vyama vya ushirika. Hatua nyingine ni kuendeleza viwanda vya ndani vya kuongeza thamani na kutafuta masoko mapya ikiwemo kuingia mikataba na nchi au wanunuzi wenye uhitaji mkubwa.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa masoko ya Kimataifa ya Kitega Uchumi ya Murongo na Nkwenda ili kuongeza chachu ya maendeleo ya Wilaya ya Kyerwa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na masoko ya Kimataifa ya kimkakati kwa ajili ya kukuza biashara na mauzo nje ya nchi kwa maendeleo na ustawi wa wananchi wake. Kutokana na umuhimu huo, Serikali imechukua hatua mbalimbali za kuhakikisha masoko ya kimkakati hususan ya mipakani yanaanzishwa, kuboreshwa na kuendelezwa.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mpaka kati ya Tanzania na Uganda, Serikali iliamua kuanzisha masoko ya kimkakati ya Kimataifa ikiwa ni pamoja na ujenzi wa masoko ya Nkwendana Murongo yaliyopo Wilaya ya Kyerwa Mkoani Kagera chini ya Mradi wa Uwekezaji wa Sekta ya Kilimo Wilayani, (DASIP) uliokuwa unafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika.

Mheshimiwa Spika, Masoko hayo bado hayajakamilika kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo ufinyu wa Bajeti. Aidha, Serikali imeunda timu ya wataalam ili kufanya uchambuzi wa kina kuhusiana na changamoto katika miradi hiyo na hatimaye kuja na mapendekezo ya namna bora ya kukamilisha ujenzi wa masoko hayo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022 Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya tathmini na uendelezaji wa masoko ya kimkakati ya mipakani. Kazi hiyo itafanywa kwa pamoja kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Wizara ya Kilimo. Aidha, Serikali inaendelea kushirikiana na wadau wengine kutafuta fedha za kukamilisha ujenzi wa masoko ya Murongo na Nkwenda kwa wakati.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutekeleza Sera ya Afya ya kuwa na Kituo cha Afya kwa kila Kata ili kupunguza vifo vya Mama na Mtoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kutekeleza Sera ya Afya ya kuwa na Zahanati kwa kila Kijiji na Kituo cha Afya kwa kila Kata kwa awamu ambapo kuanzia mwaka wa fedha 2015/2016 hadi 2020/2021 Serikali imejenga Zahanati 1,281, Vituo vya Afya 488 na Hospitali za Halmashauri 102. Mpango huu umewezesha kuongeza Vituo vya Afya katika Mamlaka za Serikali za Mitaa vyenye uwezo wa kutoa huduma za dharula za upasuaji kutoka Vituo 115 Disemba 2015 hadi Vituo 352 Juni 2021 na hivyo kuchangia katika kupunguza vifo vya mama wajawazito na Watoto. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali itaendelea na ujenzi wa vituo vya afya 121 na kiasi cha shilingi billioni 27.75 kimetengwa kwa ajili ya umaliziaji wa maboma 768 ya zahanati kote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali ni kuendelea kutenga fedha za ujenzi wa vituo vya afya kwa awamu. Nakushukuru.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawapatia maji wananchi wa Wilaya ya Kyerwa kwa kutengeneza miundombinu ya kupeleka maji kwa Wakazi waishio sehemu za miinuko?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama Wilayani Kyerwa ni wastani wa asilimia 56.8. Katika kuboresha huduma ya maji kwa wananchi wa Wilaya hiyo ikiwa ni pamoja na wale wanaoishi kwenye maeneo yenye miinuko, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi mipya ya Kagenyi - Omukalinzi na Mabila. Ujenzi wa miradi hiyo unahusisha ulazaji wa bomba umbali wa Kilometa 7.2, matenki mawili yenye jumla ya ujazo wa lita 105,000 na vituo sita vya kuchotea maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miradi hii umefikia asilimia 70 na umepangwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2022. Sambamba na miradi hiyo, Serikali ipo katika hatua za mwisho za kuajiri Wakandarasi kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya Runyinya - Chanya, Kimuli - Rwanyango na Nyamiaga - Nyakatera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hiyo, itahusisha ujenzi wa matenki matano yenye jumla ya ujazo wa lita 1,700,000, ulazaji wa mabomba umbali wa Kilometa 86.1 na ujenzi wa vituo 146 vya kuchotea maji. Kukamilika kwa miradi hiyo kutanufaisha Vijiji vya Nkwenda, Runyinya, Rwabwere, Muhurire, Karongo, Iteera, Muleba, Chanya, Chakalisa, Kagu na Nyakatera. Vijiji vingine ni Chakalisa, Kishanda, Nyakahita, Kyerwa, Nyaruzumbura, Milambi na Katera. Miradi hiyo inatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Machi, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imesaini mkataba mwezi Januari, 2022 na Mkandarasi kwa ajili ya kutekeleza mradi wa maji Kijiji cha Murongo kwa kutumia fedha za UVIKO-19. Mradi huo unahusisha ujenzi wa tenki moja la lita 150,000, ulazaji wa mabomba umbali wa Kilometa 16.6, ujenzi wa vituo 25 vya kuchotea maji. Mradi huo unatarajiwa kukamilika kabla ya mwezi Juni, 2022. Kukamilika kwa miradi yote hiyo kutaboresha upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi wa Wilaya ya Kyerwa. Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mingine ili kuhakikisha kuwa huduma ya maji safi na salama ndani ya Wilaya ya Kyerwa inafikia kiwango kisichopungua asilimia 85 mwaka 2025.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE K.n.y. MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza: -

Je, ni wananchi wangapi wameathirika na uvamizi wa wanyama wakali katika Wilaya ya Kyerwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miaka mitano, Wizara imepokea taarifa ya matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu kutoka katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa ambapo jumla ya wananchi 54 katika Vijiji vya Kibare, Businde na Nyakashenyi walipata madhara ya uharibifu wa mazao yao uliosababishwa na tembo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaiongezea TARURA fedha ili iweze kuzihudumia barabara za Wilaya ya Kyerwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikira Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kyerwa ni Wilaya ambayo kwa jiografia ina milima, miteremko pamoja baadhi ya barabara kupita katika maeneo yenye ardhi oevu. Serikali imekuwa ikitenga fedha kila mwaka kwa ajili ya matengenezo ya barabara na madaraja.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeongeza bajeti ya kuboresha miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Kyerwa kutoka Shilingi bilioni 1.39 katika mwaka wa fedha 2020/2021 hadi Shilingi bilioni 2.89. Ongezeko hili linatokana na Serikali kuongeza vyanzo vingine ambavyo ni tozo ya mafuta Shilingi bilioni 1.00, Mfuko Mkuu wa Serikali Shilingi milioni 500.00 na Mfuko wa Barabara Shilingi bilioni 1.39.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuongeza wigo wa matengenezo ya barabara pamoja na kufungua barabara mpya katika Wilaya ya Kyerwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza: -

Je, Sheria za Tanzania zinasema nini kuhusu mahusiano ya jinsia moja?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru, na kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Theonest kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria za Tanzania haziruhusu mahusiano ya jinsia moja. Kwa mujibu wa kifungu cha 9 cha Sheria ya Ndoa kinatafsiri ndoa ni mahusiano ya hiyari kati ya mwanaume na mwanamke. Aidha kwa mujibu wa kifungu cha 154 cha Sheria ya Kanuni za Adhabu, Sura ya 16 kinabainisha kuwa kufanya mapenzi kinyume na maumbile ya jinsia ni kosa la jinai ambalo adhabu yake ni kifungo cha maisha jela au kifungo kisichopungua miaka 30 jela.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza: -

Je, kiasi gani cha bajeti kimetengwa TARURA miaka mitatu mfululizo kwa ajili ya ukarabati wa barabara Kyerwa na upi ufanisi wake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa miaka mitatu mfululizo kuanzia mwaka wa fedha wa 2020/2021 hadi 2022/2023, Wilaya ya Kyerwa imetengewa jumla ya shilingi bilioni 7.34, ambapo mwaka 2020/2021 shilingi bilioni 1.26 zilitengewa, mwaka 2021/2022 shilingi bilioni 2.89 na shilingi bilioni 3.18 zimetengwa katika mwaka wa fedha wa 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, ufanisi uliopatikana ni kuwa, barabara zenye kiwango cha changarawe zimeongezeka kutoka kilomita
185.46 hadi kilometa 261.71 na barabara za udongo kupungua kutoka kilomita 711.96 hadi kilometa 634.81 na makalvati 95 yamejengwa, ikiwa ni pamoja na barabara za lami zenye urefu wa kilometa 4.2 katika Makao Makuu ya Wilaya na Mji Mdogo wa Biashara wa Nkwenda.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, Mkoa wa Kagera unachangia kiasi gani kwenye Pato la Taifa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Taarifa ya National Accounts for Tanzania Mainland inayoandaliwa na kusambazwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu, hadi kufikia mwaka 2021 Mkoa wa Kagera ulichangia 2.6% ya pato la Taifa ikilinganishwa na 2.5% ya pato la Taifa kwa mwaka 2020, ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza: -

Je, ni wananchi kiasi gani wa Wilaya ya Kyerwa wamefikiwa na huduma ya maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kulingana na Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 Wilaya ya Kyerwa ina jumla ya wananchi 368,360 ambapo kati yao wananchi 209,965 sawa na asilimia 57 wananufaika na huduma ya maji kupitia skimu 26 za maji zilizopo. Aidha, katika mwaka fedha 2022/2023 Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji ya Runyinya - Chanya, Nyamiaga – Nyakatera - Kagu, Kimuli - Rwanyango na Chakalisa. Miradi hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2023 na kuongeza idadi ya wanufaika kufikia 265,219 sawa na asilimia 72 ya wananchi wa Wilaya ya Kyerwa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali itaendelea kuboresha huduma ya maji Wilayani Kyerwa kwa kujenga miradi ya maji mipya ya Kikukuru - Mkunyu, Lubilizi, Businde - Nyakashenye, Bugara pamoja na kukarabati Mradi wa Maji Songembele. Kukamilika kwa miradi hiyo kutawezesha wananchi wote Wilayani Kyerwa kupata huduma ya maji safi, salama na ya kutosheleza. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, ni lini barabara inayotoka Karagwe kupitia Nkwenda hadi Murongo itatengenezwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY KASEKENYA MSONGWE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, zabuni kwa ajili ya kumpata Mkandarasi wa ujenzi kwa kiwango cha lami kwa sehemu ya Kyerwa hadi Chonyonyo (Kilometa 50) zimetangazwa na kufunguliwa tarehe 10 Mei, 2022. Kwa sehemu iliyobaki, Serikali ipo kwenye hatua ya manunuzi ya kumpata Mhandisi Mshauri kwa ajili ya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hiyo, ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza: -

Je, Wanawake wangapi wamekuwa Wabunge wa Majimbo na Madiwani katika chaguzi tatu mfululizo zilizopita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha kuanzia 2010 hadi 2020 zilifanyika chaguzi tatu katika ngazi ya Ubunge na Udiwani. Katika chaguzi hizo, jumla ya Wabunge Wanawake 73 walishinda chaguzi hizo na kuchaguliwa kuwa Wabunge wa Majimbo. Aidha, kwa upande wa Madiwani Jumla ya wanawake 654 waliweza kuchaguliwa na hivyo kuwa Madiwani katika Kata husika.