Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Aida Joseph Khenani (4 total)

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, dhana ya Serikali ya kutenga maeneo na kusimamia hifadhi zilizopo nchini kwetu ilikuwa ni kulinda rasilimali za nchi yetu. Sote tunajua wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi mbalimbali ni wahifadhi namba moja, jambo ambalo kwa sasa limebadilika kulingana na watendaji aidha ni wachache, kulingana na mambo yanayofanyika hivi sasa.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, natambua kumekuwa na kelele nyingi na malalamiko mengi kutoka kwa sisi Wabunge kwa wananchi wetu. Leo wananchi wanaozunguka hifadhi, wanaoshughulika na shughuli za kawaida ikiwemo kilimo, ufugaji na uvuvi, imekuwa changamoto ya kupigwa, kunyanyaswa, kunyang’anywa mifugo, jambo ambalo linakwenda kuondoa ile dhana ya wao kuwa wasimamizi wa hizi hifadhi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, miongoni mwa changamoto zinazopelekea vurugu hizo ni mipaka inayobadilishwa kila siku na mipaka mingine ambayo haieleweki, kwa maana ya kwamba havijawekwa vitu ambavyo vinaonesha alama kwamba hapa ni mpaka.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa haraka wa kwenda kupitia upya maeneo hayo ambayo yanasababisha migogoro kwa wananchi wetu ili mipaka hiyo ieleweke; na pia wanapokwenda kutengeneza au kupima hiyo mipaka, iwe shirikishi. Napenda kujua Serikali ina mpango gani wa haraka?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunayo changamoto ya uwepo wa migogoro kati ya wananchi waliopo pembezoni mwa Hifadhi zetu za Taifa, mapori tengefu ambayo yameweka ukomo wa wananchi hao kuingia kwenda huko. Migogoro hii mara nyingi imetokana na kutoeleweka kwa uwepo wa mipaka kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili Serikali imefanya jitihada kubwa; moja, ni kutoa elimu ya wananchi walioko kwenye vijiji vilivyo karibu na mipaka hii; kwanza kutambua ukomo wa mipaka ya Hifadhi hizo za Taifa na maeneo ambayo wananchi wanaishi huku wakiendelea kupata huduma za kijamii kwenye suala la uchumi na mambo mengine, kwa mfano kilimo, mifugo na shughuli nyinginezo.

Mheshimiwa Spika, uwepo wa migogoro kwenye maeneo haya ni pale ambapo kama Mbunge alivyosema, mipaka haieleweki. Jukumu hili tumeshawapa Wizara ya Maliasili kuhakikisha kwamba wanapitia ramani zilizopo na kwenda kila mahali palipo na migogoro ili kuondoa migogoro hiyo ili wananchi waweze kuishi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ameonesha kwenye Jimbo lake pia kuna migogoro ya hiyo, ndiyo sababu amekuja na swali hili. Kwa hiyo, nimuagize sasa Mheshimiwa Waziri wa Maliasili kufika Nkasi Kaskazini kuona mgogoro huo ili kutatua tatizo hilo kwa kubainisha vizuri mipaka na kuweka alama zinazoonekana zitakazomwezesha mwananchi kutokuingia kwenye eneo hilo ili kuepusha migogoro ambayo ipo. Nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba maeneo haya ya hifadhi, lakini pia mapori tengefu yanaendelezwa kwa malengo yaliyowekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunatamani kuona wananchi walipo pembezoni wakiendelea na maisha yao, shughuli zao za kijamii, kilimo, mifugo na indelezwe lakini pia kwa kuzingatia mipaka ile. Kwa hiyo, kama ni tatizo la mipaka, tayari Mheshimiwa Waziri atakuwa amepokea kauli yangu na agizo langu, aende Nkasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo Nkasi tu, na popote pale ambako kuna migongano kati ya wananchi na mipaka ili tubainishe kwa uwazi kabisa na sasa zoezi hilo liwe shirikishi; wananchi walioko jirani washirikishwe na maafisa walikuwepo pale washirikishwe, wafanye kazi kwa pamoja na kila mmoja afanye kazi yake kwa amani na watu wajipange, waongeze uchumi wao kupitia fursa zilizopo kwenye maeneo yao. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa magonjwa sugu ambayo yanakuja kwa kasi ni pamoja na ugonjwa wa Kisukari. Madaktari bingwa wanapatikana kuanzia Hospitali za Mikoa, Kanda pamoja na Taifa kulingana na Sera yetu ya Afya; na wagonjwa hawa wa Kisukari wapo maeneo yote nchini:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujua, kwa kuwa wagonjwa hao wa vijijini, wengi wanashindwa kujua kwamba wana ugonjwa huo na hawana uwezo wa kutoka vijijini na kwenda mpaka Hospitali ya Mkoa; Serikali ina mkakati gani wa ziada kulingana na uzito wa tatizo hili hivi sasa kuweza kutoa huduma kwenye Hospitali za Wilaya pamoja na ngazi ya Kata?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nami naungana naye kwamba tunayo magonjwa mengi nchini na ambayo tunaendelea kutafuta tiba sahihi ili Watanzania waendelee kuwa na afya njema zitakazowawezesha kufanya shughuli zao za maendeleo. Ugonjwa wa Kisukari ni miongoni mwa magonjwa ambayo kwa sasa yamesambaa sana nchini. Kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, ni kweli mengine yapo mpaka kwenye Vitongoji.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu imepanua wigo wa utoaji huduma za afya. Wigo huu umeanzia kwenye ngazi ya huko huko vijijini ambapo kuna zahanati. Vile vile katika ngazi ya Kata kama rufaa ya zahanati, tuna vituo vya afya vinavyotoa huduma nzuri sana sasa hivi na tumejenga vituo vya afya vingi sana na tunaendelea kuvijenga. Pia tuna Hospitali za Wilaya, Mkoa na Rufaa mpaka zile za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ugonjwa wa Kisukari ni miongoni mwa magonjwa ambayo sasa tunatoa huduma mpaka kule kwenye zahanati. Kwenye Sera yetu imeelekeza zahanati na zenyewe zinunue madawa ya Kisukari ili wawe wanapata huduma kule. Pale ambapo anaweza kupimwa kwenye Hospitali ya Kata ambayo ipo kwenye maeneo hayo hayo, lakini upatikanaji wa dawa sasa unakwenda mpaka kwenye zahanati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni jukumu la zahanati na nataka niagize Halmashauri ambazo ndiyo zinasimamia zahanati kuhakikisha kwamba wanaagiza dawa za Kisukari na ziende katika zahanati, kwenye kituo cha afya na kwenye kila ngazi ya kutoa huduma ili wale Watanzania walioko kule kijijini kabisa wapate huduma hiyo bila usumbufu wa kusafiri na kulipa nauli kwenda mahali pengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kupitia Mheshimiwa Aida, nikuhakikishie kwamba Serikali tumejipanga vizuri kwenye sekta ya utoaji huduma kwenye ngazi zote na bado tunaendelea na maboresho ya utoaji huduma kwa magonjwa yote. Mkakati wetu sasa ni kuhakikisha tunapunguza ukali wa magonjwa haya ili Watanzania wawe na afya njema na kila Mtanzania afanye kazi yake vizuri. Tunataka tuone tija ikipatikana kwa Watanzania kuwa na fya njema.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2017 Serikali ilikuja na utaratibu wa upigaji chapa kama eneo la kutambua mifugo nchini. Zoezi hilo lilikuwa na changamoto zake ikiwepo chapa hizo kupotea au kufutika pamoja na ngozi kukosa ubora. Kupitia Bunge lako Tukufu, Bunge liliitaka Serikali kuja na namna bora ya utambuzi wa mifugo. Mwaka huu Serikali imekuja na utaratibu mpya wa kuvalisha hereni mifugo; zoezi ambalo limeanza tarehe 17 mwezi wa Nane mwaka huu kwenye baadhi ya mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hilo ni zuri kwa sababu lina barcode ya nchi, mkoa, wilaya na jina la mfugaji. Hata hivyo, changamoto kwenye zoezi hilo ni pamoja na gharama ya shilingi 1,750 kwa kila ng’ombe. Lakini ng’ombe huyo akipoteza hereni mfugaji analazimika tena kulipia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nia ya Serikali ni njema na itakwenda kuondoa wizi wa mifugo uliopo sasa hivi. Serikali haioni kuwa ni vyema iende ikafanye tathimini upya ione namna bora kwanza kupunguza gharama lakini kuona namna bora wataweka hiyo hereni na isiweze kuondoka kwenye mifugo? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imetafuta njia nzuri sana ya kufanya maboresho ya utambuzi wa mifugo yetu, ng’ombe wakiwemo. Na mfumo huu ulitokana na tatizo kubwa sana la wizi wa mifugo hapa nchini pamoja na kukosa takwimu sahihi za mifugo yetu hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetafuta njia kadhaa za kuweza kutambua na kupata takwimu za ng’ombe hawa. Awali tulikuwa tunatumia njia ya kupiga chapa, lakini tumegundua kwa kupiga chapa tunapoteza ubora wa ngozi ambapo ngozi zetu sasa nchini Tanzania haziuziki nje; na hata tulipoanza kutumia Kiwanda chetu cha Kilimanjaro Leather kwa kutengeneza viatu, ngozi zote zilizopigwa chapa hazitumiki vizuri kwa sababu zenyewe zimepoteza ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumetafuta njia nzuri ya kuweza kutambua hawa ng’ombe, tukaamua kutumia njia ya kuvalisha hereni. Kwanza mwanzo tulikuwa tunatoboa lakini sasa hatutoboi bali tunaibandika. Inawezekana pia ng’ombe mmoja mmoja kutokana na kupita kwenye majani na miti hereni zinadondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia kikao cha juzi cha mifugo ambacho mimi mwenyewe nilikuwa mgeni rasmi na mjadala uliofanyika kwenye kikao kile juzi pale Jijini Dar es salaam, kwenye eneo hili Wizara ya Kilimo wameondoa hizo tozo; endapo ulinunua kwa mara ya kwanza na sasa ng’ombe amepoteza herein. Tunachofanya ni kurudi tena kwenye mtandao na kujaza zile data zote kwenye hereni mpya tunampa mfugaji ili ng’ombe aendelee kuwa na ile alama aendelee kutambulika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hatua nzuri ya kumuondolea gharama mfugaji ni hiyo ya kumrudishia tena ile hereni ili aweze kuivaa. Pili, hereni hii tumekuwa makini sana, hatutoboi tena bali tunatafuta namna ya kuigandisha vizuri pamoja na ile spring inabana vizuri kiasi kwamba hata akiwa na pilikapilika haiwezi ikadondoka kwa urahisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaendelea kutafuta njia nzuri zaidi ya hiyo. Niseme sasa kwamba tumepokea mawazo yako, na uzoefu ambao tumeuona kupitia wafugaji wetu kwamba hizi zinadondoka na kunakuwa na shida tena kurudi ofisini kupata hereni nyingine, kwa hiyo tunatafuta njia nzuri zaidi ya kutambua ng’ombe hawa kwa kuweka alama ambayo haitaharibu ubora wa masikio ya ng’ombe lakini pia haitasababisha gharama tena kwa mfugaji ili gharama ile ile aliyoitumia kwa mara ya kwanza iendelee kutumika kama alama ya kumtambulisha ng’ombe huyo. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, lakini nashukuru kwa kauli ya Serikali ambayo imetolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili la uvalishaji hereni kwa ng’ombe lilianza katika Mkoa wa Rukwa, Wilaya Nkasi, na ikafikia mahali mpaka kutishwa kwa wafugaji, na mimi Mbunge nikalazimika kwa sababu ilikuwa ni kauli ya Serikali, nikapita kuwahamasisha wafugaji kutii maagizo ya Serikali na wakatoa hiyo fedha ya shilingi 1,750. Leo kuna maeneo ambayo yalikuwa hayajafikiwa; kwa kuwa ni utaratibu mzuri mlileta ninyi upigaji chapa siyo wafugaji, Serikali ilitoa hayo maagizo na wafugaji wakalipa, leo likaja agizo lingine la uvalishaji hereni wametii.

Mheshimiwa Spika, naomba kujua, kwa kuwa ni nia njema ya Serikali, kwa wale ambao walikuwa tayari wameshalipa hiyo fedha, itakuwaje ili na wao wajione ni sehemu ya wafugaji wengine wa Tanzania?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hatujasitisha malipo, tumesitisha zoezi hili ambalo linalalamikiwa ili kuipa nafasi Serikali kupitia Wizara ya Mifugo kufanya tathmini ya mapungufu ya kanuni iliyowekwa ili kuweza kufanikisha zoezi hili vizuri kwa kushirikisha na wadau. Kama kutakuwa na maamuzi mengine ndani ya Wizara ya kupunguza bei, fedha, itakuwa ni baada ya mjadala huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa sasa tumesitisha tu zoezi lenyewe kuendelea, kwa sababu tangu sheria imewekwa mwaka 2010 na kanuni zake mwaka 2011, kati ya mifugo milioni 45 ni mifugo milioni tano tu mpaka leo kuanzia mwaka 2011 ndiyo imefanikiwa kufikiwa. Kwa nini? Maana yake kuna tatizo. Kama tungetekeleza inavyotakiwa leo tungefikia angalau nusu ya mifugo yote nchini kuwekwa hereni.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumesema tunasitisha kwa muda wa miezi mitatu, ili kuipa nafasi Wizara kukaa ndani ya Wizara yenyewe, kupitia kanuni zao kuona wapi kuna dosari zilizosababisha kutofanikiwa kupata mifugo mingi zaidi, lakini kupitia hayo malalamiko ambayo yanawafanya wafugaji au kukwepa au kutoshiriki vizuri au kujiunganisha vizuri na watendaji walio kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa ambao ndio wanatakiwa kuwatambua watu wao kila Wilaya ili sasa kuweka mfumo mzuri unaowezesha kufikia hatua nzuri zaidi na kuondoa manung’uniko yanayotokana na utekelezaji ambao unaonekana si mzuri.

Mheshimiwa Spika, baada ya januari, sasa hayo mambo yote, maazimio yote yatakayokuwa yamefikiwa, ili waweze kufanya vizuri wakati wa utekelezaji yataanza kuanzia tarehe 1 Februari, 2023. (Makofi)