Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Zainabu Nuhu Mwamwindi (7 total)

MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI aliuliza:-
Baadhi ya vyuo vikuu nchini vinaendelea kufanya tafiti mbalimbali zenye manufaa kwa wananchi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuviwezesha vyuo vikuu vyote hapa nchini, vikiwemo vya Tumaini na Mkwawa kufanya tafiti zitakazosaidia jamii kubwa ya wananchi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Zainabu Nuhu Mwamwindi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia mwaka wa fedha 2010/2011, Serikali iliazimia na kuanza kutenga kiwango kikubwa cha fedha za utafiti ikilinganishwa na miaka ya nyuma ili kuhakikisha kuwa tafiti zinafanyika kulingana na vipaumbele vya kitaifa. Serikali imekuwa ikitenga fedha hizi kupitia Mfuko wa Taifa wa Uendelezaji wa Sayansi na Teknolojia (MTUSATE) unaoratibiwa na Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kulingana na Sheria Namba 7 ya mwaka 1986 iliyoanzisha Tume hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za utafiti kutoka kwenye mfuko huu zimekuwa zikitumiwa na watafiti wa ndani ya nchi wakiwemo watafiti kutoka vyuo vikuu. Utaratibu ni kwamba miradi hii ya utafiti hufadhiliwa kwa misingi ya ushindani kupitia ubora wa maandiko ya miradi ya utafiti. Hivyo basi, vyuo vikuu vyote vikiwemo Vyuo Vikuu vya Tumaini na Mkwawa vinayo nafasi ya kupata fedha hizo iwapo vitaomba na kukidhi vigezo husika vya ushindani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, vyuo vikuu vyote vinatakiwa kutenga fedha kupitia bajeti zao pamoja na kutafuta wafadhili, wadau wa maendeleo kwa ajili ya kuendeshea shughuli mbalimbali za maendeleo, ikiwemo kufanya utafiti.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI aliuliza:-
Gereza la Wilaya ya Iringa ambalo lipo jirani na Hospitali ya Mkoa wa Iringa limekuwa likisababisha usumbufu kwa wananchi wanaotembea kwa miguu hasa nyakati za usiku.
Je, Serikali ina mpango gani kwa kuondoa mwingiliano wa shughuli za kijamii na shughuli za gereza hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Nuhu Mwamindi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yalikuwepo malalamiko ya wananchi kupata usumbufu wa kuingia na kutoka Hospitali ya Mkoa wa Iringa ambapo barabara ya kuingia inapita mbele ya lango la Gereza la Iringa. Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Iringa katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo, hasa baada ya kufungwa kwa barabara inayopita mbele ya gereza kuelekea hospitalini kwa watumiaji wa magari ilikutanisha uongozi wa Manispaa ya Mkoa wa Iringa na uongozi wa Jeshi la Magereza mkoani humo na kutoa maangizo yafuatayo:-
Moja, uongozi wa Manispaa ya Iringa kuandaa barabara mbadala itakayotumiwa na wananchi wanaokwenda hospitalini kwa kutumia gari; pili, uongozi wa Manispaa uandae ramani ya ukuta utakaozuia matumizi ya barabara inayopita gerezani kwa kutumia gari. Ukuta huo ulilengwa kuzuia magari kutoka eneo ambalo waenda kwa miguu wangepita bila kuingilia shughuli za gereza; na tatu, baada ya kupatikana ramani, uongozi wa gereza ulitakiwa kujenga ukuta huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza tayari limeshatekeleza maagizo hayo kwa kujenga ukuta unaotenganisha barabara ya watembea kwa miguu wanaokwenda hospitali kwa kutumia eneo la mbele ya gereza ili wasiingiliane na shughuli za gereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Halmashauri ya Manispaa ya Iringa imeshatekeleza agizo la kujenga barabara mbadala inayotumiwa na wananchi wanaokwenda hospitalini na magari. Hata hivyo, pamoja na kujengwa kwa barabara mbadala, gereza limeendelea kuruhusu magari yanayokwenda hospitalini kutumia barabara hiyo mbele ya gereza kwa wakati wa dharura.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI aliuliza:-
Zahanati ya Kalenga iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa haikidhi mahitaji halisi ya wakazi wa vijiji vinavyoizunguka.
Je, ni lini Serikali itaboresha zahanati hiyo kwa kujenga vyumba vya ziada na mahitaji mengine ya msingi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Nuhu Mwamwindi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Zahanati ya Kalenga ilijengwa zaidi ya miaka 40 iliyopita. Kutokana na ongezeko la watu, kwa sasa zahanati hii imekuwa ikitoa huduma kwa wananchi ambao wamekuwa wengi kuliko ilivyokuwa hapo awali. Hata hivyo, Halmashauri haiwezi kuongeza majengo kwenye eneo la zahanati hii, kwani tayari imezungukwa na makazi ya watu, hivyo hakuna nafasi ya kuongeza majengo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto hiyo, baadhi ya vijiji vilivyokuwa vinapata huduma kwenye zahanati hii, vimejengewa zahanati ambayo ni zahanati ya Mangalali iliyofunguliwa mwezi Februari, 2017. Zahanati hii imesaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa katika zahanati ya Kalenga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, juhudi zinafanyika kwa kuhamasisha ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Jirani ya Mlanda. Ujenzi huu unafanyika kwa nguvu za wananchi na upo katika hatua za awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri katika mpango wa bajeti wa mwaka 2018/2019 imetenga kiasi cha shilingi milioni 54 ili kufanikisha ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Mlanda. Kituo hicho kitakapokamilika, kwa kiasi kikubwa kitapunguza msongamano wa wagonjwa katika Zahanati ya Kalenga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuziagiza Halmashauri zote nchini kutenga maeneo ya kutosha kwa ajili ya Taasisi za Umma kama vile shule, vituo vya kutolea huduma za afya na Ofisi za Vijiji, Mitaa, Kata na kuhakikisha maeneo haya yanapimwa na kupatiwa Hati Miliki ili kuondoa changamoto zinazoweza kujitokeza siku za usoni.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI aliuliza:-
Shule ya Msingi Kipela, Wilayani ya Iringa, inahudumia wanafunzi wenye mahitaji maalum (albinism) lakini haina miundombinu rafiki, watumishi wa kutosha, huduma za afya stahiki na umeme:-
Je, lini Serikali itarekebisha mapungufu hayo?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Nuru Mwamwindi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shule ya Msingi Kipela ina jumla ya wanafunzi 701 wakiwemo wanafunzi 93 wenye mahitaji maalum ambao wote wanakaa bweni. Shule hii ina hitaji la walimu wataalam wa elimu maalum 17 ambapo kwa sasa wapo walimu 7 na hitaji la watumishi wasio walimu 13, kwa sasa wapo 7. Vilevile shule hii ina mahitaji ya vyumba vya madarasa 16 kwa sasa vipo 12.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shule ya Msingi Kipela ipo umbali wa kilometa 8 toka Makao Makuu ya Kata ya Mzihi ambapo ndiko kuliko na umeme wa gridi ya Taifa kwa sababu hiyo, kwa sasa shule hii inatumia umeme wa jua (solar). Aidha, shule inapata huduma za afya kwenye Zahanati ya Kanisa Katoliki iliyopo jirani na shule. Huduma hii, huchangiwa kwa malipo kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na miundombinu ya shule hiyo, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imepeleka jumla ya shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa bweni rafiki na la kisasa kwa ajili ya wanafunzi hao. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na wadau wengine wa elimu itaendelea kuboresha miundombinu hiyo pamoja na shule zingine za aina hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na ajira, Serikali ipo kwenye mchakato wa kuajiri walimu wa shule za msingi 4,785 wakiwemo walimu wa mahitaji maalum. Shule ya Msingi Kipela ni miongoni mwa shule za wanafunzi wenye mahitaji maalum zitakazopangiwa baadhi ya walimu hao.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI aliuliza:-

Udumavu na Utapiamlo mkali ni tatizo kwa watoto wengi nchini:-

Je, Serikali ina mpango gani unaotekelezeka wa kukabiliana na hali hiyo ikiwemo kuzijengea uwezo Kamati za lishe za kata?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Nuhu Mwamwindi Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeazimia kutekeleza malengo la Baraza la Afya Duniani (World Health Assembly) la kutokomeza utapiamlo ifikapo mnwak 2025, pamoja na kutekeleza maazimio mbalimbali ya kupunguza utapiamlo ya kitaifa kikanda na Afrika Mashariki. Kitaifa, Serikali kupitia sera ya Taifa ya afya mwaka 2007 ambayo kwa sasa inapitiwa imeeleza wazi kuwa itaboresha huduma za lishe kwa wananchi wake. Kwa miaka ya karibuni Serikali imeongeza juhudu katika kupambana na tatizo la utapiamlo nchini kwa kushirikiana na wadau wetu wa maendeleo wa ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juhudi mbalimbali zilizofanyika ni pamoja kuandaa na kutekeleza mpango mkakati jumuishi wa kitaifa wa Utekelezaji wa Afya za Lishe (National Multi-sectoral Nutrition Action Plan ya mwaka 2016/ 2017 ambayo itaisha mwaka 2021/2022 ambayo una vipaumbele vinavyolenga kupunguza utapiamlo kufikiapo mwaka 2021 ambavyo ni pamoja na:-

(i) Kupunguza viwango vya hudumavu kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka 5 kutoka asilimia 34 mawaka 2015 hadi 28.

(ii) Kudhibiti viwango vya ukondefu kwa watoto wenye umri chini ya miaka 5 na kufanya viendelee kubakia chini ya asilimia 5 iliyopo sasa.

(iii) Kupunguza viwango vya watoto wanaozaliwa na uzito pungufu kutoka asilimia 7 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 5.

(iv) Kupunguza idadi ya wanawake walio katika umri wa uzazi miaka 15 - 49 wenye upungufu wa damu kutoka asilimia 44.7 kwa mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 33.

(v) Kupunguza tatizo la upungufu wa vitamin A kwa watoto wenye umri wa miezi 6 hadi miezi 59 kutoka aslimia 33 hadi kufikia asilimia 26.

(vi) Kudhibiti tatizo la uzito uliozidi kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano na kubakia chini ya asilimia 5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilianzisha muundo wa kada ya Maafisa Lishe chini ya Wizara ya afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto mwaka 2012 ambapo jumla ya Maafisa Lishe 114 wameajiriwa katika mikoa na halmashauri za Serikali. Sanjari na hilo, Wizara ya Afya na Ofisi ya Rais - TAMISEMI ipo katika mchakato wa kuangalia utaratibu wa kuajiri wahudumu wa afya, ngazi za jamii angalau wawili wawili kila kijiji ambapo pamoja na shughuli nyingine watatoa huduma za lishe katika ngazi ya kaya.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO (K.n.y. MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI) aliuliza:-

Ubunifu wa kupata ajira ni miongoni mwa changamoto kubwa kwa vijana hapa nchini:-

Je, ni lini Serikali itabuni na kusimamia mkakati wa kuwajengea uwezo wa kujiajiri vijana kuanzia shule za msingi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Nuhu Mwamwindi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa mkakati wa kuwajengea uwezo wa kujiajiri vijana kuanzia elimu ya msingi ni muhimu kutokana na kuwa vijana wanapomaliza elimu ya msingi hususan ambao hawaendelei na masomo wanaingia moja kwa moja katika soko la ajira. Kutokana na umuhimu huu, Serikali imeandaa miongozo ya kufundisha masuala ya ujasiriamali na imeanza kutoa mafunzo ya ujasiriamali kuanzia shule za msingi hadi vyuo vya elimu ya juu. Mafunzo ya ujasiriamali yatawezesha vijana kuweza kuibua miradi na kuitekeleza na hatimaye kuajiri wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeandaa Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza Ujuzi nchini pamoja na Programu ya Kukuza Ujuzi. Lengo ni kuhakikisha kuwa vijana wa Kitanzania wanapata ujuzi na stadi za kazi stahiki ili kuwawezesha kujiajiri au kuajiriwa. Kupitia Programu ya Kukuza Ujuzi nchini wameendelea kupata mafunzo kupitia taasisi na vyuo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2018/2019 jumla ya vijana 32,563 wamewezeshwa kupata mafunzo ya ujuzi wa kujiajiri na kuajiriwa katika sekta mbalimbali. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 jumla ya vijana 47,000 watapata mafunzo ya stadi za kazi mbalimbali ikijumuisha mafunzo ya ujasiliamali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuimarisha Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kwa kutenga fedha katika bajeti kila mwaka ambazo zinalenga kusaidia vijana kujiajiri na kuwapa mikopo ya masharti nafuu na mafunzo ya ujasiriamali mali. Aidha, kutokana na mabadiliko ya sheria yaliyopitishwa na Bunge lako Tukufu, Serikali za Mitaa zinatenga asilimia 10 ya mapato yake ya ndani katika kuwawezesha vijana ili waweze kujiajiri ambapo asilimia 4 ni vijana, asilimia nne ni wanawake na hata vijana wanawake na asilimia mbili ni kwa vijana wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuimarisha mikakati mbalimbali iliyopo ya kuwajengea uwezo vijana kujiajiri pamoja na kubuni mikakati mingine zaidi ili kuhakikisha kuwa vijana wetu wanapata ajira.
MHE. ZAINAB N. MWAMWINDI aliuliza:-

Katika kuboresha utalii katika Hifadhi ya Ruaha:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa kiwango cha lami barabara iendayo Hifadhi ya Ruaha pamoja na kuimarisha miundombinu ya ndani ya Hifadhi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Nuhu Mwamwindi Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza mipango ya kukamilisha ujenzi wa barabara iendayo Hifadhi ya Taifa ya Ruaha yenye urefu wa kilomita 130 kwa kiwango cha lami. Hadi sasa, kipande cha barabara hiyo kutoka Iringa mjini hadi Kalenga chenye urefu wa kilometa 14 kimeshajengwa kwa kiwango cha lami. Sambamba na ujenzi wa barabara hiyo, pia miundombinu ya ndani ya Hifadhi ya Taifa Ruaha inaimarishwa.

Mheshimiwa Spika, jukumu la ujenzi wa barabara zilizoko nje ya hifadhi ni la Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini TARURA na Wakala wa Ujenzi wa barabara TANROADS. Wizara itaendelea kufuatilia kwa karibu mamlaka zinazohusika ili kuzishawishi ziweke barabara hiyo katika Mpango Kazi wa uendelezaji wa barabra za Mkoa.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Shirika la Hifadhi za Taifa ina utaratibu wa kufanya ukarabati wa miundombinu ndani ya hifadhi za wanyamapori kila mwaka, pamoja na kuongeza miundombinu mipya pale inapohitajika. Hifadhi ya Taifa Ruaha, ina mtandao wa barabara za utalii zenye urefu wa takriban kilometa 1,590. Hifadhi ya Taifa Ruaha kupitia mpango wake kukuza na kuendeleza utalii Kanda ya Kusini REGROW imepanga kukarabati na kufungua barabara za utalii zenye urefu wa kilometa 1,055 katika kipindi cha miaka mitano ya mradi huo.