Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Flatei Gregory Massay (2 total)

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya uhakiki wa watumishi ambao wana vyeti fake. Sasa baada ya uhakiki huo wengine wameacha vituo vya afya na zahanati zetu kule.

Sasa swali langu, je, lini mtaajiri sasa, ili watu wetu kule wapate huduma, hasa kwenye maeneo ya afya ambako watumishi wameshaacha kazi kutokana na kwamba, walikuwa wana vyeti ambavyo havistahili kuendelea kuwepo? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumepitisha zoezi hili la uhakiki wa vyeti kwa watumishi wetu na uhakiki huu baada ya kuwa tumekamilisha tulipata makundi matatu. Kundi la kwanza ni wale wenye vyeti fake moja kwa moja, kundi la pili ni wale wenye vyeti vinavyotumika na zaidi ya mtu mmoja, lakini kundi la tatu uko utata wa majina ambao umejitokeza kwenye vyeti hivi ambavyo wao wamepata nafasi ya kukata rufaa. Sasa wote hawa wameacha pengo kwa sasa, na ndilo ambalo Mheshimiwa Mbunge amelizungumzia, lini tunatoa ajira.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli ametoa nafasi za ajira zaidi ya 50,000 ili kuziba mapengo haya ambayo yamejitokeza kwa wenye vyeti fake, lakini vilevile ili kuongeza tu ajira kwenye sekta nyingine kwa lengo la kuboresha utoaji huduma kwenye sekta mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, tayari vibali vimeshatolewa na Wizara ya Utumishi, tumeanza na idara ya elimu, tumesha ajiri walimu wa masomo ya sayansi wamekwenda kwenye vituo, tumetoa pia nafasi kwenye sekta ya afya na vibali hivi vitaendelea kutolewa kadri ya nafasi ambazo Mheshimiwa Rais ameahidi kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, ninaamini Rais wetu mpendwa kwa ahadi yake nafasi hizi ataendelea kuzitoa ili tuzibe mapengo na kuboresha pale ambako kuna upungufu mkubwa. Na sasa ajira hizi zitaenda kitaaluma zaidi, ili kuweza kuleta ufanisi mkubwa kwenye sekta y ajira. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali kwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pamekuwa na wizi wa ng’ombe uliokithiri katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Mfugaji mara nyingi anapopata tatizo lolote anatumia ng’ombe wake kumsaidia na hao ng’ombe wamekuwa wakitolewa mkoa mmoja hadi mwingine pamoja na kuwa na chapa hizi alizozijibu katika swali la mwanzo.

Je, Serikali ina kauli gani kuhusiana na wizi huu?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kudhibiti wizi wa mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Watanzania wote kwamba vyombo vyetu vya ulinzi nchini vimeendelea kufanya kazi kubwa sana na nzuri ya kudhibiti matukio ya uhalifu kote nchini ikiwemo la wizi wa mifugo na matukio mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la mifugo tunaendelea na udhibiti huo na tumetafuta njia rahisi ya kuweza kupunguza matukio haya. Moja, ni ile njia ambayo nimeijibu muda mfupi uliopita ya kuweka alama mifugo hii ili iweze kutambulika ni ya nani, ya eneo gani ili pale inapopotea tunaweza kuipata. Pia, tumeendelea kushirikisha wananchi kwenye ulinzi shirikishi kwa matukio yote ikiwemo wizi wa mifugo na wa namna nyingine yoyote ya uhalifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujaishia hapo, tumeendelea pia kushirikiana na wafugaji hawa kuhakikisha kwamba tunaweza kuimarisha ujenzi wa maeneo wanayoishi mifugo hii kwa mfano maboma yao, tumekuta maeneo mengine maboma yao wanazungusha tu miiba peke yake lakini ni rahisi ng’ombe hata kuruka na kuondoka na baadaye tunasema wameibiwa lakini kumbe boma lile siyo imara sana. Kwa hiyo, tumeendelea kutoa elimu ya uimarishaji wa maeneo hayo wanayohifadhiwa ng’ombe ili kuzuia wizi na wakati mwingine ng’ombe wenyewe kutoroka.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, tumedhibiti sana vibali vya usafirishaji holela kutoka eneo moja mpaka eneo lingine. Kama mwizi anaiba ng’ombe eneo A anawapeleka eneo B bila ya ukaguzi inakuwa ni rahisi sana sasa tulichofanya ni kudhibiti usafirishaji wa ng’ombe kutoka eneo moja mpaka lingine. Sasa ng’ombe hawezi kuhama kutoka kijiji kimoja mpaka kingine bila ya kibali maalum kinachotambulisha mwenye mifugo na kule anakokwenda. Hii ndiyo ambayo inasimamiwa sana kwa sasa ili kuweza kupunguza wizi wa mifugo kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kutoa elimu kwa wafugaji lakini tunaendelea pia kufanya mikutano ya wafugaji kama nilivyosema ili haya mengine yote yanayojitokeza katika udhibiti wa wizi wa mifugo yaweze kupungua kwa kiasi kikubwa huku vyombo vya ulinzi vikiendelea na kazi yake ya ulinzi. Ahsante sana. (Makofi)