Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Zainab Athuman Katimba (30 total)

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na nitambue kazi kubwa inayofanywa na Wizara hii katika utekelezaji wa majukumu yake, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti mfumo wa uhakiki wa vigezo vinavyotumika kutoa mikopo kwa wanafunzi, ili kuhakikisha wanaopata mikopo ni wenye sifa na uhitaji na sio wale ambao wanafanya udanganyifu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha mfumo huu wa utoaji mikopo utaendelea kuwa himilivu na endapo idadi ya wanafunzi itaendelea kuongezeka?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Bodi inatakiwa kuhakikisha kuwa kumbukumbu za wote wanaoomba mikopo zinakuwa kamilifu kwa kushirikiana na vyuo ambavyo vina wanafunzi wanaopewa mikopo hiyo. Kila chuo kinatakiwakuwa na dawati maalum ambalo linashughulikia mikopo, lakini pia katika kutoa mikopo ni lazima kuzingatia vigezo na sifa ambazo zimewekwa. Hivi karibuni Wizara imepitia vigezo hivyo na vigezo vinazingatia hasa uhitaji, uraia, lakini pia uombaji lazima upitie kwenye mtandao na vilevile kwa kuzingatia mahitaji ya nchi, yaani kipaumbele katika taaluma ambazo zinahitajika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kuona kwamba, mikopo hiyo inakuwa endelevu ni kwamba, Wizara baada ya kuangalia matatizo yaliyokuwa yakijitokeza katika ulipaji wa mikopo, imeangalia upya Sheria ya Bodi ya Mikopo na hivyo tuko katika kutaka kuileta Bungeni, ili kuona kwamba, inarekebishwa kuweka mikopo kuwa ni deni la kipaumbele kwa mwombaji ambaye ameshamaliza chuo. Lakini vilevile kuhakikisha kuwa waajiri wanahusika nao moja kwa moja katika kuhakikisha mikopo hiyo inalipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika sambamba na hiyo tunaangalia namna ya kuboresha upya mifumo mizima ili kuona mfumo huo unaweza kuongea na taasisi nyingine zinazohudumia raia, ikiwemo ya Vitambulisho vya Taifa. Ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA:Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.
Serikali ina mpango kabambe wa kupima na kurasimisha ardhi nchi nzima na imekuwa ikishirikisha sekta binafsi katika kufanya hivyo. Aidha, kumekuwa na gharama kubwa sana katika upimaji na urasimishaji huo wa ardhi. Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya mapitio ya gharama hizo ili kuweza kuwapunguzia wananchi mzigo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Zainab anazungumzia habari ya gharama kubwa katika suala zima la upimaji. Lakini naomba nimkumbushe tu bajeti ya mwaka jana ilivyosomwa gharama zile zilishuka kutoka shilingi 800,000 kwa heka mpaka shilingi 300,000 kitu ambacho ilipunguza sana gharama zinaongezeka kulingana na ukubwa wa eneo ambalo linaenda kupimwa. Kwa mwaka huu pia katika bajeti yetu nadhani kuna maeneo ambayo Serikali imeyafanyia kazi mtayasikia wakati tunatoa bajeti.
Kwa hiyo, niseme kwamba gharama tunaziangalia
na namna bora ya kuweza kumuwezesha mwananchi wa kawaida aweze kupima ardhi yake na kuweza kumiliki ili kumletea maendeleo katika shughuli zake.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii niulize swali la nyongeza.
Kwa niaba ya vijana wote wa Tanzania ambao wanaweza kuwa wanufaika wakubwa sana wa michezo naomba kuuliza swali la nyongeza lifuatalo:
Je, Serikali haioni umuhimu wa kwamba ni wakati muafaka wa kuwa na shule maalum kwa ajili ya kukuza vipaji katika michezo kama sports academy? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Ninampongeza kwa kuwatetea vijana kimichenzo, kama alisikiliza vizuri hotuba ya Mheshimiwa Waziri wakati akiwasilisha bajeti yake ya mwaka 2017/2018 ni kwamba tumedhamiria. Serikali sasa hivi imekwishatenga shule takribani 55 ambazo ziko katika Mikoa yote ya Tanzania, hizi ndizo ambazo tutazichukulia kama ndizo academy zetu. Vilevile michezo ya UMISETA, michezo ya UMITASHUMTA itasaidia sana kuibua vipaji, hata hivyo tunashirikiana sana na Wizara ya Elimu kuhakikisha kwamba michezo inafundishwa katika ngazi zote za elimu tangu awali, sekondari na vyuoni. Ahsante. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na niseme ninatambua jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano katika kuboresha elimu. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Je, Serikali ina mkakati gani katika mabweni haya 155 ambayo inatarajia kuyajenga katika mwaka wa fedha 2017/2018 kuhakikisha kwamba, inazingatia kipaumbele katika ujenzi wa mabweni katika shule zetu za kata?
La pili, je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Mamlaka ya Elimu ya Juu Tanzania ambayo inaonekana inapata changamoto kutokana na kutokuwa na fedha za kutosha, inatengewa fedha za kutosha ili iweze kutekeleza majukumu yake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutekeleza mkakati wa kujenga mabweni kwa kushirikiana na Halmashuri na wananchi, kama ambavyo tumekuwa tukifanya na hivi natoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge wote kule kwenye maeneo yao ambako kuna ujenzi wa mabweni, basi wasaidie kuwahamasisha wananchi washiriki kikamilifu kwenye mkakati huu, lengo ni kuhakikisha kwamba, tunakamilisha ifikapo mwezi Juni mwakani, kama ambavyo tumejipanga.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, tutaweka fungu maalum kwenye bajeti kwa ajili ya kuisaidia taasisi ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja pamoja na taasisi nyingine ambazo zinasaidia maendeleo ya elimu nchini. Ahsante sana.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali imefanya jitihada gani ili kuhakikisha kwamba wavuvi wanaweza kuzifikia na kunufaika na hizi fursa alizozizungumzia Mheshimiwa Naibu Waziri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha inasimamia kwa ukamilifu sekta hii ya uvuvi ili kuhakikisha inaepusha uvuvi haramu ambao utaleta uharibifu kwa mazingira?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ni jitihada gani ambazo Serikali imeshakufanya. Kama nilivyojibu katika swali la msingi ya kwamba, la kwanza, tumeendelea kuhamasisha wavuvi kujiunga katika vikundi mbalimbali ili waweze kutumia fursa zinazojitokeza, kama vile fursa niliyoitaja ya ruzuku ambapo katika mwaka huu wa 2017/2018 tumeshatenga shilingi milioni 100 ili kuweza kuendelea kuwasaidia wavuvi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Sheria ile ya Fedha ya mwaka 2007 tunaendelea kuisimamia kuhakikisha ya kwamba zana za uvuvi zinaendelea kupatikana kwa bei nafuu. Pia tunalo dirisha katika Benki yetu ya Rasilimali ambalo linahusu wakulima, wavuvi na wafugaji ili waweze kupata mikopo mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni juu ya hatua gani Serikali inachukua kukomesha uvuvi haramu ili kulinda rasilimali zetu. La kwanza kabisa Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wavuvi na jamii za wavuvi ili kulinda rasilimali zetu kwa ajili yetu na vizazi vijavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali imejishirikisha katika kufanya doria mbalimbali ambazo zimeleta matunda chanya ya kuhakikisha kwamba uvuvi haramu unapigwa vita ikiwa ni pamoja na uvuvi wa matumizi ya mabomu na uvuvi wa nyavu zisizoruhusiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho katika kupambana na uvuvi haramu, Serikali inakusudia kuleta maboresho ya Sheria yetu ya Uvuvi Namba 22 ya mwaka 2003 ili kuipa meno zaidi kuhakikisha tunaendelea kulinda rasilimali za nchi yetu. Nashukuru sana.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Ninaswali moja la nyongeza. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba ina hakikisha wavuvi hawa wanapata sokola uhakika baada ya kuhamasisha uzalishaji kwa kuhakikisha kwamba kuna jengwa kiwanda cha kuchakata minofu ya samaki katika ukanda wa Lake Tanganyika na hasa ukizingatia kwamba kuna specie ya kipekee katika Ziwa Tanganyika ya samaki anayeitwa migebuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali ina mkakati gani kuhakikisha viwanda vinajengwa katika ukanda ule? (Makofi)
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI:Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu wa uvuvi katika Ziwa Victoria tumejenga mwalo wa kisasa pale Kibirizi ambapo mwalo ule tumeuwekea vifaa vyote muhimu ambavyo samaki akivuliwa anaweza kutunzwa hata kwa zaidi ya wiki mbili. Yote haya ni kuwafanya wavuvi wanapovua samaki kabla hawajafika sokoni wasiharibike yaani waweze kupata soko kabla hawajaharibika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais tumejenga pale mradi mkubwa sana wa ziadi ya takriban shilingi bilioni mbili zimetumika kwa ajili ya kutengeneza mwalo ule.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hili la pili linalokuja ni la kujenga viwanda sasa kwa sababu tayari tumeshapata mwalo mzuri ambapo samaki wanapokelewa na kutunzwa. Kinachofuata sasa ni maandalizi ya kujenga kiwanda ili tuweze kuchakata samaki katika ukanda ule na tutafanya hivyo. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali lakini pia nashukuru kwa kuchukua ushauri wangu. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mkakati wa kufikia uchumi wa viwanda unalenga pamoja na mambo mengine kutatua changamoto ya ajira hususan kwa vijana, na kwa kuwa viwanda vya ngozi nchini vinakabiliwa na changamoto ya kodi kubwa katika malighafi ya kuchakata ngozi.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa tax incentives kwa viwanda vinavyozalisha mazao yanayotokana na mifugo ili kufikia malengo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, Serikali haioni haja ya kuwa na breeding program ili kuongeza kiwango na ubora wa mazao yanayotokana na mifugo Tanzania. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako naomba sasa nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba na naomba nimpongeze sana kwa maswali yake mazuri yanayolenga katika kuhakikisha kwamba Tanzania ya viwanda inapatikana lakini pia tunazalisha ajira kupitia sekta yetu muhimu ya mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza linaeleza juu ya suala la kufanya mkakati au Serikali ina mkakati gani wa kuweza kuvipendelea viwanda vyetu vya ndani katika tasnia ya ngozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yetu tayari imeshapeleka mapendekezo Wizara ya Fedha ya kuhakikisha kwamba kodi zote zinazotozwa katika accessories za uchakataji wa ngozi ziweze kupunguzwa ama kuondolewa kabisa ili kusudi kuweza kuhamasisha uwekezaji zaidi kwenye tasnia hii ya ngozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo tumehakikisha tunapendekeza Wizara ya Fedha iweze kuongeza viwango kwa bidhaa za ngozi zinazotoka nje ya nchi kuingia nchini hasa za mitumba ili kusudi kuweza ku- discourage uagizaji wa bidhaa hizo na uwekezaji zaidi ufanyike ndani ya nchi yetu, na huu ndio mtazamo wetu kama Wizara ya Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili linahusu mpango mkakati wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wa kuweza kupata mifugo bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mpango wa kuhamasisha, tunaita artificial insemination au uhimilishaji wa mifugo yetu na hii tumefanya kwa kuanzisha vituo maeneo mbalimbali takriban vituo sita katika nchi, na tunacho kituo kikubwa sana pale Arusha cha NAIC pale Usa River ambacho kinazalisha mbegu bora. Vilevile zile mbegu zinatawanywa katika hivyo vituo vingine vilivyopo kote nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na mkakati huo tumekuwa tukinunua mbegu bora hata kutoka nje ilikuweza kuja kuongeza ubora wa mifugo yetu tuliyonayo hapa nchini. Vilevile tunakwenda katika kuhakikisha kwamba tunaboresha sheria yetu ya mbali za mifugo ili kusudi kuweza kwenda sambamba na mabadiliko hayo tunayoyataka ya kuboresha mifugo yetu hapa nchini ili tuweze kupata nyama bora na tuweze kupata maziwa bora na kwa wingi, ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nilipenda tu niongezee, kwanza nilitaka nithibitishe kwamba mapendekezo yaliyotoka Wizara ya Mifugo ni kweli yamefika Wizara ya Fedha na hapa mkononi mwangu nina bangokitita lina kurasa 53 ya mapendekezo ya maboresho ya kodi mbalimbali zikiwemo hizi za tasnia ya mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Zainab avute subira kidogo Serikali itaji- pronounce kupitia hotuba kuu ya Serikali. Nimuhakikishie kwamba kabisa ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba viwanda vyetu vya ndani vinapewa ahueni ya kodi mbalimbali kadri itakavyowezekana. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda kwanza kutambua kazi kubwa inayofanywa na Serikali katika kuelekea katika uchumi wa viwanda, lakini ningependa kuuliza swali moja la nyongeza. Changamoto zinazokabili zao hili la tangawizi ni zilezile ambazo zinakabili zao la mchikichi.
Je, Serikali haioni ni wakati wa kuendelea kuongeza nguvu kuhamasisha wakulima waweze kuongeza uzalishaji wa michikichi na kujengwe kiwanda cha kuchakata na kusindika mawese ili kuweza kuongeza kipato kwa wakulima na kuleta manufaa kwa Taifa hili?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo, mpango wa Serikali kwa Mkoa wa Kigoma ni kuainisha kaya 100,000 ambapo kila kaya itapanda michikichi na tunawasiliana na Wabunge wa Kigoma akiwemo Mzee Nsanzugwanko na Mheshimiwa Peter Serukamba ili tuweze kupata vikonya vya kupandikiza kutoka nchi za Malaysia ambazo zitatumia kituo cha Arusha kuzalisha vikonya zaidi kusudi tuzalishe miche ya michikichi tuwagawie wananchi kwa bei nafuu tofauti na shilingi 5,000 ambazo mnanunua mchikichi, tunakuja Kigoma.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Kwanza ningependa kutambua jitihada kubwa sana zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Dkt. John Pombe Magufuli katika vita dhidi ya madawa ya kulevya na ningependa kuwatia moyo na waweze kuendelea na jitihada hizi. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, je, Serikali haioni kwamba kuna haja ya kuweka katika mitaala ya elimu ya msingi pamoja na sekondari mafunzo kuhusu athari ya dawa za kulevya?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, je, hawa vijana 3,000 waliopatiwa tiba katika kipindi cha miaka 10 iliyopita kwa kushirikiana na wadau, je Serikali inafahamu vijana hawa wako wapi katika muda huu, yaani kwa sasa na wanafanya nini?(Makofi)
WAZIRI WA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI:
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ningependa kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Katimba kuhusiana na kipengele cha mpango wa Serikali kuweka kwenye mitaala masuala ya madawa ya kulevya.
Mheshimiwa Spika, ningependa kusema kwamba mitaala ya kuanzia shule za msingi, Sekondari pamoja na masuala ya kitaaluma lakini pia inakuwa imebeba masuala mtambuka. Kwa hiyo, masuala yanayohusiana na masuala ya madawa ya kulevya, masuala ya jinsia, masuala ya UKIMWI yapo katika mitaala yetu na tutaendelea kuyaimarisha ili kuhakikisha kwamba tunaenda sambamba na azma ya Serikali ya kupambana na hili janga la madawa ya kulevya nchini. Ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, pia nashukuru kwa kuchukua mapendekezo haya na kuona umuhimu wa kutunga sera hii ya mafunzo kwa vitendo kazini kwa wahitimu.
Mheshimiwa Spika, nina swali moja la nyongeza, sisi tunafahamu kwamba ili kijana/mhitimu awe na uzoefu, uzoefu hujengwa kwa kuanza. Sasa pamoja na kwamba Serikali itatunga sera hii kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo kazini kwa wahitimu, lakini haioni haja kwamba kuna kazi zingine ambazo hazihitaji kuwa na experience, kwa sababu ukiangalia leo hii ajira zilizotolewa utakuta kuna kigezo, two years experience, three years experience, five years experience. Sasa hawa vijana wanaohitimu, wataanza lini kupata huo uzoefu kama kila kazi inayotolewa inahitaji wawe na uzoefu?
Mheshimiwa Spika, sasa pamoja na kwamba Serikali itatunga sera hii ambayo itaweza kusaidia kuondoa hilo umbwe kati ya elimu waliyopata wahitimu pamoja na mahitaji ya soko la ajira lakini Serikali haioni haja kwamba kuna kazi zingine ambazo hazihitaji huo uzoefu na vijana waweze kupata fursa ya kuajiriwa ili na wenyewe waweze kujikwamua na changamoto ya kukosa ajira? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTONY P. MAVUNDE): Mheshimiwa Spika, naomba kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Zainab Katimba kwa namna ambavyo anawapigania vijana wa Taifa hili la Tanzania na vile alivyokuwa mstari wa mbele kuhakikisha maslahi ya vijana yanalindwa katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwepo na changamoto kubwa katika masuala ya uhitaji wa uzoefu katika nafasi za kazi ambazo zimeombwa na kama itakumbukwa, wakati wa kampeni mwaka 2015 Mheshimiwa Rais pia aliwahi kulisema hili juu ya kigezo hiki cha uzoefu. Sisi kama Wizara tukaona kwa sababu asilimia kubwa ya vijana wanaotoka katika Vyuo Vikuu na Vyuo vya Elimu ya Juu wamekuwa wakipata taabu sana kwenda kujifunza kivitendo na wengi wao ni mashahidi huwa wanatembea na ile barua ya to whom it may concern na wengine mpaka kumaliza soli za viatu bila kupata eneo la kwenda kufanyia kazi. Kama Serikali tukaona sehemu ya kwanza ya kuanzia ni kuhakikisha tunatengeneza mwongozo huu na mwongozo huu tumefanya kati ya Serikali, waajiri na Vyama vya Wafanyakazi ili tutoe nafasi kwa vijana wale wahitimu wa Vyuo Vikuu wakimaliza masomo yao na tumeshazungumza na haya makampuni yatoa nafasi, tunawapeleka moja kwa moja katika makampuni na taasisi mbalimbali kwenda kujifunza kuanzia miezi sita mpaka mwaka mmoja. Lengo letu ni kuondokana na kikwazo cha kigezo cha experience ili akitoka pale akienda sehemu awe ana reference.
Mheshimiwa Spika, hili ni eneo la kwanza ambalo tumelianzia, naamini kabisa kupitia mpango huu utawasaidia sana vijana wasomi wa nchi yetu ambao wamekuwa wakipata tabu na kikwazo cha uzoefu. Kwa hiyo, hivi sasa atapata nafasi ya kujifunza katika kampuni kwa muda huo wa mwaka mmoja na baadaye tutampatia cheti cha kumtambua ili iwe kama reference yake katika sehemu inayofuata. Tunafahamu ni tatizo kubwa, ni changamoto kubwa lakini kama Serikali tumeona tuanzie hapa kwenda mbele na jinsi Waheshimiwa Wabunge watakavyotushauri tutaona namna nzuri ya kuboresha mpango huu.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, naomba kuongeza majibu machache katika swali hili na hasa nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo amekwisha kuyasema.
Mheshimiwa Spika, baada ya Serikali kuona tatizo hilo Mheshimiwa Naibu Waziri amesema tumeshatengeneza hiyo miongozo. Tunafikiri sasa kazi yetu kubwa ambayo tumeanza kuifanya ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu ni kuji-link sisi Ofisi ya Waziri Mkuu na miongozo tuliyonayo na wenzetu wa Wizara ya Elimu, lakini kupitia vyuo vikuu vyote kuhakikisha kwamba tunatambua mahitaji na tunawasaidia hawa vijana kuwaandaa vizuri, ili awingie kwenye soko la ajira.
Mheshimiwa Spika, tumekubaliana pia ndani ya Serikali na ndio maana mmeona hata ajira na matangazo ya ajira yanayotolewa sasa hivi, ajira hizo zinazotolewa sasahivi kwa kweli, kimsingi wengi wanaoajiriwa kwenye ajira hizi ni wale ambao ni fresh kutoka kwenye vyuo vyetu vikuu na taasisi nyingine ambazo zinatengeneza ujuzi. Wakati mwingine tunaweza kuwa tunataka ajira katika position fulani ambazo zina matakwa rasmi. Kwa mfano, Mkurugenzi labda wa kitu fulani kwa matakwa fulani kwa hiyo, huko ni lazima tuone sasa wale walioenda internship, lakini vilevile wale ambao wana uzoefu katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie vijana wetu kwa kweli, baada ya kuona hiyo gap ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu tumeifanyia kazi vizuri sana, sasa hivi waajiri na Serikali kwa pamoja na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi tumeanza kulifanyia kazi vizuri sana eneo hilo. Na tunawaondoa hofu vijana wetu kwa kweli sasa tunataka kuwapa assurance ya ajira bila kupata vikwazo vyovyote katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi hii ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa jitihada za kutoa mitaji kwa vijana na wanawake inabidi ziende sambamba na kuwajengea uwezo wa kuanzisha na kuendeleza biashara. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwatumia hawa Maafisa Biashara katika kuwajengea uwezo vijana wanaokuwa katika vikundi ambao wananufaika na asilimia 10 inayotengwa kutoka kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri? Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kwa dhati kabisa nimshukuru na kumsifu sana Mheshimiwa Zainab Katimba kwa sababu yeye amekuwa anashughulikia sana sana maslahi ya vijana katika Bunge hili Tukufu. Aliwahi kuleta mpaka mapendekezo ya hoja kutaka kutetea vijana wanaomaliza shule ili kusudi waajiriwe bila kuwa na experience. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimhakikishie kwamba vijana katika nchi hii wana idara nyingi sana za kuweza kuwasaidia mawazo ya kujikwamua kutoka pale walipo kwenda mbele. Katika Halmashauri kuna Idara ya Vijana, Idara ya Maendeleo ya Jamii na Idara ya Mipango sasa Maafisa Biashara tunawongezea sehemu nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana nitumie nafasi hii kuwaomba vijana wa nchi hii ambao hata fursa ambayo ziko katika Halmashauri hawazitumii ipasavyo, ukienda katika Halmashauri unakuta maombi ya vijana yako asilimia 10 ya maombi yote yaliyowasilishwa. Kwa kweli, naomba sana Waheshimiwa Wabunge tujitahidi kuwaelimisha na kuwaomba vijana wajitokeze na wajiunge katika vikundi na watumie fursa zilizopo kwa ajili ya kujiendeleza na Serikali tuko macho katika kuangalia suala hilo linatekelezwa vizuri. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwanza nianze kwa kupongeza maamuzi ya Serikali ya kutoa elimu bure kwa shule za msingi na shule za sekondari na sisi wote ni mashahidi ni kwa namna gani maamuzi haya yameweza kuleta tija kwa Taifa letu. Aidha, nina maswali mawili ya nyongeza.

Kumekuwa na matukio ya adhabu za kuchapa wanafunzi zilizopitiliza mashuleni ambazo zimesababisha madhara makubwa ya kisaikolojia na kwa wakati mwingine zimesababisha vifo vya wanafunzi. Japokuwa kuna mwongozo wa namna gani adhabu hizi za kuchapa...

SPIKA: Mheshimiwa Zainab swali.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Okay, japokuwa kumekuwa na mwongozo wa namna ya kutumia adhabu hii ya kuchapa wanafunzi mashuleni lakini mwongozo huu umekuwa hauzingatiwi.

Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na masuala haya ya adhabu mashuleni?

Swali la pili, je, wenzetu ambao wamefanikiwa katika sekta ya elimu walifanikiwa kwa sababu ya kuwapo kwa adhabu hizi za kuchapa wanafunzi mashuleni au walifanikiwa kwa sababu ya kuwekeza katika mifumo, mitaala pamoja na miundombinu ya ufundishaji?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba utekelezaji wa kanuni na waraka unaohusiana na viboko bado haujafuatwa kikamilifu. Kwa hiyo, naomba nitumie nafasi hii kuwataka viongozi wote wanaosimamia elimu pamoja na walimu, kuhakikisha kwamba wanafuata Waraka ule Namba 24 wa mwaka 2002, lakini vilevile Kanuni ile inayofahamika kama The Corporal Punishment Regulations wa mwaka 2002.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ifahamike kwamba kwa wale walimu ambao hawatafuata waraka na kanuni hiyo,
wanakuwa wanafanya kosa na wanaweza kuchukuliwa hatua za kinidhamu kwa mujibu wa sheria inaitwa The Teacher Services Act ya mwaka 1989 kama ilivyorejewa mwaka 2002. Kwa hiyo, nawataka wote wafuate taratibu hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake la pili kwamba wenzetu wamefanikiwa vipi kuboresha elimu bila kutumia adhabu ya viboko.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge, pamoja na Wabunge wengine ni kwamba viboko havitumiki Tanzania pekee, hata Marekani huko ambapo ndio tunafikiri wameendelea sana majimbo 19 kati ya majimbo 50 ya Marekani mpaka leo hii yanatumia viboko. Naomba nimwambie kwamba Serikali haitumii tu viboko kama njia ya kuboresha elimu, kuna mengine mengi tunafanya, tunaendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia, viboko ni sehemu ndogo tu na tena tunatumia kidogo sana. Kwa hiyo asije akafikiri kwamba sisi tunatumia viboko tu. Kwenye hilo la viboko hatupo peke yetu duniani tunafahamu mtindo wowote wa kufundisha lazima uhusishe adhabu na zawadi (punishment and rewards).
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali na natambua jitihada kubwa sana zinazofanywa na Serikali katika kuongeza uzalishaji wa umeme lakini nina swali moja tu la nyongeza. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhamasisha na kuwezesha kisera uwekezaji wa miradi midogo midogo ya uzalishaji wa umeme hususan katika maeneo ambayo hayajafikiwa na gridi ya Taifa kama vile Mkoa wa Kigoma?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri katika swali la msingi la Mheshimiwa Katimba. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia wazalishaji wadogo wadogo katika nishati kwa upande wa maeneo ambayo hayana gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, Serikali kama ambavyo tumeeleza katika jibu la msingi, pamoja na kuzalisha umeme mkubwa katika maeneo mbalimbali yenye gridi ya Taifa, bado Serikali inahamaisha sana uzalishaji wa umeme mdogo mdogo katika maeneo ambayo hayajafikiwa na gridi ya Taifa. Katika maeneo ya Kigoma mathalani; wazalishaji wadogo wameshajitokeza, Kampuni ya Nexgen Solar White imeanza kuzalisha megawatts tano ambazo sasa wanafanya majadiliano na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kuingiza kwenye gridi ya Taifa. Kwa hiyo ni matumaini yetu maeneo mbalimbali ya Ujiji ambayo yameshafanyiwa utafiti kwenda mpaka Kaliua kuja mpaka Mkoa wa Tabora wazalishaji wataongezeka zaidi.

Mheshimiwa Spika, katika kuongeza maelezo ya upana zaidi kwenye suala la nyongeza la Mheshimiwa Katimba ni kwamba katika maeneo ya Mkoa wa Kigoma na Uvinza ambayo hayajapitiwa na umeme wa gridi ya Taifa, hivi sasa Serikali imeanza kujenga njia ya kusafirisha umeme mkubwa wa gridi ya Taifa ili Mikoa ya Kigoma na Katavi nayo ifikiwe na gridi ya Taifa. Sasa hivi ujenzi unaanzia Tabora kupitia Jionee Mwenyewe-Juhudi-Nguruka mpaka Kidawe Mchini-Kigoma, kwa hiyo, hata wazalishaji wadogo wa umeme mdogo mdogo nao wataingizwa kwenye gridi ya Taifa.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu kwamba kuna changamoto kubwa sana ya ukatili kwa wanawake, ikiwemo na watoto kwenye masuala ya ubakaji. Nasi tunafahamu kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inataka kuwahakikishia usalama Watanzania wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye makosa ya ubakaji, kama ilivyoainishwa kwenye Kifungu cha 5 cha Sheria ya Sexual Offences Special Provisions Act ya Mwaka 1998 ambayo imeenda kufanya marekebisho ya Kifungu cha 130 cha Sheria ya Adhabu (Penal Code), tunaona kwamba, kigezo au masharti ya kuthibitisha kosa la ubakaji ni mpaka yule aliyebakwa athibitishe kwamba kulikuwa kuna kuingiliwa (penetration). Mazingira hayo ni magumu sana katika utaratibu wa kawaida kuthibitisha kwamba mtu amekuingilia, yani ku- prove penetration siyo kitu kirahisi na hasa kwa watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo ni swali la kwanza. Nataka kufahamu: Je, Serikali haioni katika mazingira haya kwamba kufanyike marekebisho ya sheria, ili standard of proof au ili kuthibitisha kosa la ubakaji ipunguzwe kiwango chake ili kusiwe kuna haja ya ku-prove penetration kwa sababu, watoto siyo rahisi kwao kuweza kuthibitisha jambo kama hilo, lakini mazingira yote kiujumla ya kosa hilo yaangaliwe ili kuweza kutoa haki. Hilo swali la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Je, Serikali haioni kwamba kuna haja ya kuongeza adhabu kwa wale watakaothibitika kwamba wamefanya kosa la ubakaji ili adhabu yao iwe kali ili kuhakikisha kwamba makosa haya ya ubakaji yanakwisha na watu
waogope?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Serikali haioni kwenye kosa la ubakaji, mbakaji apewe adhabu ya kuhasiwa ili asije akarudia tena kufanya kosa kama hilo ambalo linaleta ukatili mkubwa sana kwa wanawake na watoto na linawaathiri kiasi kwamba, hata kama mtu amechukuliwa hatua, bado wale ambao wameathirika wanapata athari kwa muda mrefu zaidi? Nashukuru.
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kusimamia haki za watoto na hasa wanawake katika kutoa ushahidi kwenye makosa ya aina hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza katika majibu yangu nimesema, la kwanza tumeondoa baadhi ya vigezo ambavyo vilikuwepo vya hasa watoto kuweza kutoa ushahidi wenyewe na kuachia Mahakama uamuzi wa busara na wa kitaalam kuweza kutoa ushuhuda huo kama kitendo hicho kimetokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nimesema katika jibu langu kwamba sasa hivi kuna mfumo wa kutazama na kuboresha mfumo mzima wa kesi za jinai. Na katika hilo litakuwa hilo lingine linalohusiana na ubakaji; na kama itatoa mapendekezo, nina hakika pia mapendekezo hayo yatafuatana na adhabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie kweli kwamba, kwa makosa haya adhabu ambazo zipo mpaka sasa, ni kali na inafika mpaka miaka 30 na mmejadili katika Bunge hili. Kama itabidi kuongeza adhabu hizo baada ya marekebisho na mapitio ya sheria hizi, ninashauri kwamba Bunge hili likae na tushauriane na tuweze kuzungumzia suala hili. Linahitaji uamuzi wa kisheria kama tunataka kufanya adhabu kali zaidi kuliko zilizopo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshuhudia mwenyewe Magerezani kuwaona watu wenye makosa kama haya wamepewa adhabu ya miaka 30 na wengi wao pengine watafia Magerezani. Ahsante sana. (Makofi)

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba tu niongezee katika majibu mazuri sana aliyotoa Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria. Kuhusu swali la nyongeza la kwanza la Mheshimiwa Zainab kwamba bado vigezo inaonekana ni vikubwa sana katika kuthibitisha makosa; napenda tu kumwambia kwamba katika ile Sheria ya Sexual Offences Special Provisions Act ilipopitishwa, mojawapo ya masuala iliyoyaondoa kwenye Sheria ya Ushahidi ilikuwa ni ile requirement ya colaboration. Colaboration ilikuwa ni lazima uoneshe kwamba kuna ishara fulani zilizosalia baada ya lile tendo la ubakaji na hiyo ilikuwa inadhalilisha. Kwa hiyo, sheria hiyo iliondoa kitu hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa siku ni lazima haya yote yafuate misingi ya sheria za jinai, kwamba, lazima kuthibitisha pasipo kuacha shaka ili pia anayetuhumiwa asije akatuhumiwa isivyo sahihi au akapewa adhabu isivyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili suala la kuongeza adhabu, tayari sheria ile kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri, imeongeza adhabu imekuwa kali sana ni miaka 30. Sasa hili pendekezo la kuhasiwa lina tatizo moja, litatusababisha kuvunja Katiba, kwa sababu, Ibara ya 13(6) inaeleza kwamba ni marufuku kwa mtu kuteswa, kuadhibiwa kwa kinyama au kupewa adhabu zinazomtweza au kumdhalilisha. Kwa hiyo, tukichukua pendekezo la kuhasiwa linatupeleka tena katika upande mwingine ambapo tutaweza kuvunja Katiba. Nafikiri adhabu zilizopo zinajitosheleza kwa sasa. Ahsante.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama sambamba na majibu mazuri ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri wa Katiba na Sheria na swali zuri ambalo ameliuliza Mheshimiwa Zainab Katimba. Nilitaka tu kuweka mkazo. Sheria peke yake, hata tuwe na sheria kali kiasi gani hatutamaliza tatizo la ubakaji na ulawiti wa watoto na wanawake nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimesimama hapa kuendelea kutoa msisitizo kwa wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kutimiza wajibu wetu wa malezi na ulinzi wa watoto. Inasababisha mtoto anabakwa miezi mitatu bila mzazi kujua. Unajiuliza hivi huyu mtoto ana wazazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, narudisha mzigo kwa wazazi na walezi tutimize wajibu wetu, tuwafuatilie watoto wetu, tuwakague watoto wetu, tuwaulize watoto wetu, tujenge urafiki wa watoto wetu kutueleza changamoto na matatizo ambayo wanayapata. Tutaweka sheria kali, wazazi wata-negotiate na wabakaji mwisho wa siku hakuna hatua ambazo zitachukuliwa. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali na Serikali kuonesha ina nia ya kusaidia kwenye masuala ya mawasiliano, lakini sote tunafahamu sasa hivi kuna zoezi la usajili wa namba za simu kwa alama za vidole na zoezi hilo linahitaji kuwepo au kuwa na kitambulisho cha Taifa na ukomo wa zoezi hilo ni tarehe 31 Desemba, 2019. Je, Serikali kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani ina mkakati gani wa kuhakikisha wale ambao hawajapatiwa vitambulisho vya NIDA hasa hasa wananchi wa Mkoa wa Kigoma wanapatiwa hivyo vitambulisho vya NIDA ili itakapofika tarehe 31 Desemba, 2019 Watanzania wote wapate haki ya kuendelea kufanya mawasiliano? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Katimbaa, Mbunge, Kundi la Vijana kutoka Mkoani Kigoma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Zainab Katimba kwa jinsi anavyopambana kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata mawasiliano katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Zainab kwamba tumejipanga kama Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wanawasiliana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kujibu swali lake, ni kweli kwamba kumekuwa na changamoto ndogo za mwanzo wakati tunaanza zoezi hili tarehe Mosi, Mei, 2019 kuhusu suala la upatikanaji wa vitambulisho vya NIDA na sisi kwa upande wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, hatuhitaji kitambulisho cha NIDA, tunahitaji namba ya NIDA kwamba unapokwenda kusajili pale unapewa namba maalum. Kitambulisho kinaweza kikachelewa kwa njia moja au nyingine, lakini sisi tunachohitaji ni namba, ukishapata ile namba unakwenda kwa watoa huduma za mawasiliano unasajili kwa alama za vidole. Ni kweli kwamba sehemu mbalimbali watu wamekwishaenda kujisajili na namba zinaendelea kutolewa mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa ninavyoongea Watanzania milioni 12,783,000 tayari wameshasajili kati ya watu milioni 44 ambao kwa takwimu za Serikali zinaonesha kwamba wana line za simu. Kwa hiyo naendelea kuwasisitiza na kuwaomba Watanzania tusisubiri mpaka mwisho, mtu mwenye namba ya kitambulisho aende akasajili kwa alama za vidole ili angalau itakapofika tarehe 31 Desemba, tutakapokuwa tumeizima mitambo yetu yeye asikose mawasiliano.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini nilikuwa nadhani kuna haja ya Serikali kuwa mfano katika ujenzi wa majengo yake kwa kuweka miundombinu ya uvunaji wa maji kwa mfano kwenye majengo ya hospitali, shule, zahanati na kadhalika. Aidha, nina swali moja la nyongeza. Pamoja na jitihada hizi za kubuni mbinu mbalimbali za uvunaji maji ya mvua, bado kuna uhitaji wa maji katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Kigoma, yakiwemo maeneo ya Mwandiga:-

Je, Serikali inatuambia nini au inawaambia nini wananchi wa Mwandiga kuhusiana na upatikanaji wa maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokitaka kuwahakikishia wananchi wa Mwandiga, mimi nimekwishafika pale na Mheshimiwa Waziri amefika, tumetuma fedha kiasi cha shilingi milioni 400. Tumeagiza wataalamu wetu wa ndani wafanye ile kazi. Mpaka sasa uchimbaji wa mabomba wameshachimba, lakini pia mabomba yameshafika pale na tutajenga tenki zaidi ya lita 150,000 katika eneo la Bigabilo katika kuhakikisha wananchi wa Mwandiga wanapata safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Aidha, nina swali moja la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama vile Serikali ilivyoona umuhimu wa kuanzisha Mahakama kwa mfano za Kazi (Labor Courts) au Mahakama za Mafisadi (Economic Crimes Courts) au Commercial Courts (Mahakama ya Biashara) kwa ajili tu ya kutengeneza mazingira wezeshi ya kiuchumi lakini pia ya uwekezaji. Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kuanzisha Divisheni ya Familia (Family Division) katika Mahakama itakayoshughulika na masuala ya ndoa, talaka na mirathi ili kuharakisha mashauri haya na kuwaondolea wanyonge adha wanayopata ya kuchelewa kwa mashauri haya katika mfumo wa kawaida wa mahakama na hasa ukizingatia wanyonge hao ni wajane? Sisi tunajua kuna legal maxim ambayo inasema justice delayed is justice denied (haki iliyocheleweshwa ni sawasawa na haki iliyonyimwa). (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab, Mbunge Viti Maalum kutoka Kigoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wake ni mzuri sana na chombo hiki ndiyo chombo chenye kazi ya kutunga sharia kwani sheria zote zinatungwa hapa Bungeni. Tusema tu tumepokea wazo lake na tutalipitisha katika mamlaka mbalimbali za kuangalia ile modality ya kuanzisha chombo kama hiki ili tuweze sasa kufikia maamuzi halisi. Naamini Bunge lako Tukufu litapata nafasi ya kupitia na kutoa maoni mbalimbali juu ya muundo utakaowezesha kutoa haki kwa makundi husika. Ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Kama Serikali ilivyosema kwamba imetoa utaratibu mzuri wa kwamba mtu anayeanzisha biashara awe ana miezi Sita kabla ya kuanza kulipa kodi, lakini sasa katika uhalisia (in practice) mazingira hayapo hivi. Mpaka sasa bado watu wanatakiwa. Kwa sababu mtu anapoanzisha biashara inabidi kwanza apate leseni ya biashara ili apate leseni ya biashara inabidi aende akapate TIN na ili apate TIN inabidi apate TAX Clearance, sasa ili apate hiyo TAX Clearance anapewa makadirio ya kodi na analazimika alipe robo ya kwanza ya yale makadirio ya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa analipa kabla hata ya hiyo miezi Sita ambayo amepewa kama muda ambao hatakiwi kulipa kodi. Sasa naomba kujua kwa sababu ni mwongozo na ni utaratibu ambao umetolewa na Serikali lakini kiuhalisia haupo hivyo.

Je, Serikali inatoa majibu gani kuhusiana na changamoto hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Athman Katimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hili tulichukue tulifanyie uchunguzi, lakini nitoe maelekezo kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania kufuata Sheria, Utaratibu na Kanuni zilizowekwa na Serikali. Ahsante. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu ya Serikali yanayotia faraja. Nina swali moja la nyongeza. Naomba kufahamu na kauli ya Serikali kuhusiana na kukamilika kwa ujenzi wa barabara hii ifikapo mwaka 2025.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi tunayoitekeleza sasa hivi na imeeleza wazi kwamba lazima tuifanyie usanifu wa kina. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Mheshimiwa Makanika ambaye amekuwa akiifuatilia sana hii barabara kwamba tutahakikisha tunaifungua yote na baada ya hapo tutaanza kuifanyia usanifu wa kina baada ya kukamilisha upembuzi yakinifu wa barabara hii.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Kwa kuwa wanawake wa Kigoma wanaojishughulisha na uvuvi wanahitaji kujengewa uwezo katika mnyororo wa thamani na kuongezewa pia mitaji. Je, ni lini Serikali italeta mradi huu ili uweze kuwanufaisha wanawake wa Mkoa wa Kigoma wanaojishughulisha na shughuli za uvuvi. (Makofi)
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Kigoma na Ukanda wote wa Ziwa Tanganyika, tuna mradi unaoitwa Fish for ACP ambao unajumuisha Ukanda wote wa Ziwa Tanganyika. Lengo la mradi huu ni kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi kwenye Ziwa Tanganyika ikiwemo dagaa, migebuka na mazao mengine ya uvuvi yaliyoko kwenye Ukanda wa Ziwa Tanganyika. Mradi huu unalenga kuongeza ubora, unalenga kupunguza upotevu wa mazao ya uvuvi unaotokea kwenye mialo na kwenye masoko yalioko kwenye ukanda huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tayari, Serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi huu na mwaka huu tutaendelea; na miaka mingine tutaendelea mpaka ukanda uliye...

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa majibu mazuri.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Nashukuru sana kwa majibu ya Serikali amefafanua vizuri kabisa madhara yanayotokana na wenza kutokuwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, ukiangalia athari ambazo zinatokana na wenza kutokupata nafasi ya kufanya kazi wakiwa wako pamoja, ni kubwa sana na zinaathiri jamii; na sisi tunajua kwamba familia bora ndiyo inajenga jamii bora. (Makofi)

Sasa ni nini mkakati wa Serikali wa kukabiriana na hili suala lililopo mbele yetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, ni nini kauli ya Serikali kwa waajiri wale ambao hawatoi fursa ya kuhakikisha kwamba wafanyakazi wao wanapata haki ya kufanya kazi wakiwa karibu na wenza wao?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zainab kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza linahusu madhara ambayo yanawapata watoto wakati wenza wao mbalimbali. Serikali kupitia MTAKUWWA imeunda Kamati Maalum za kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake kwa ngazi zote. Maafisa wetu wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii wanapita kuelimisha kwa njia za vyombo vya habari, mikutano na makongamano mbalimbali pamoja na midahalo ya kitaifa ambayo inaendelea kila mkoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili, nini tamko la Serikali kuhusu wenza ambao wanakatazwa kuwafuata wenza wao walipo. Kanuni na sheria zipo ambazo zinaeleza kila kitu katika Serikali. Serikali yetu imeunda sera, kanuni na miongozo ambayo inawaelemisha wananchi kufuata sheria zitakazowafanya wapate vibali vya kwenda kukaa na wenza wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maelezo zaidi napenda kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge tujifunze kukaa na watoto wetu wakati wowote ule kuwapa muda maalum ambao tunaweza kuwaelimisha elimu ambayo Serikali yetu na utamaduni wetu. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake ambayo yameonesha msingi wa hoja hii muhimu sana ya kuhakikisha kwamba ustawi wa familia kwa maana ya wenza na watoto kuishi pamoja ili kuweka makuzi bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilihakikishie Bunge lako tukufu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma inadhamana ya kuangalia ustawi wa watumishi wote nchini. Baada ya kutambua tatizo hili la wenza kukaa maeneo tofauti tofauti na kusababisha kuwa na athari kubwa katika malezi ya familia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ameshatoa Waraka Namba 452501 kifungu cha 6(b) kimetoa masharti ya kumhakikishia mtumishi ana uwezo wa kuomba kibali cha kuhamia kwa mwenza wake endapo eneo husika litakuwa na nafasi na atakuwa na uthibitisho wa vyeti vya ndoa na nyaraka nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nitoe wito kwa waajiri wote kuhakikisha wanazingatia kifungu cha waraka huo ili kusaidia ustawi wa familia, malezi ya watoto na kuhakikisha kwamba wafanyakazi wetu wanakuwa na fursa ya kuishi na wenza kwa kuzingatia taratibu na miongozo iliyowekwa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Nataka kufahamu Je, Serikali ni kwa kiwango gani inatakeleza mkakati wa hifadhi na matumizi endelevu ya maji, kama vile kujenga au kutengeneza miradi ya uvunaji maji ya mvua kama vile ilivyoainishwa kwenye ukurasa 36, 37(a)(3) cha Ilani ya Chama cha Mapinduzi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Katiba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miundombinu ya mabwawa ndani ya Wizara ya Maji, kwa sasa tuna mabwawa Sita ambayo yako kwenye utekelezaji, lakini tuna sanifu mbalimbali ambazo zinaendelea na nyingine zimekamilika na katika utekelezaji huo, tayari tunatarajia kuwa na bwawa kubwa la Kidunda, ambalo wenzetu wa DAWASA chini ya uongozi wa Cyprian tayari wamepata kibali cha kuweza kwenda kumpa kazi Mkandarasi pamoja na Mhandisi Mshauri na hawa wote wameshaenda kuoneshwa site na tunarajia lile Bwawa la Kidunda liweze kuwa ukombozi mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa hapa Dodoma Bwawala Farkwa na lenyewe pia tunaendelea kulifanyia kazi ili liwe ni jibu sahihi la miradi kuwa endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo yote ya nchi tunatarajia kuchimba mabwawa mengi. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan ameweza kuruhusu zaidi ya shilingi bilioni 34 tunazitumia kwa ajili ya kuleta mitambo seti Nne kwa ajili ya kuchimba mabwawa, vilevile seti 25 za kuchimba visima na seti za kufanya utafiti wa maji chini ya ardhi ziko nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mitambo hii yote kuwasili nchini Waheshimiwa Wabunge, tutafikia Majimbo yote kwa urahisi na suala la kuvuna maji ya mvua litapewa kipaumbele na kuona kwamba linaenda kuleta uendelevu wa miradi.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, kuna dawa ambazo zinanunuliwa bila cheti cha daktari, (over the counter medication) na kuna dawa zile ambazo ni lazima uwe na cheti cha daktari, ili uweze kununua, (prescription medication).

Je, Serikali inafanya jitihada gani na ina mikakati gani thabiti ya kuhakikisha kwamba, zile dawa ambazo zinahitaji cheti cha daktari hazinunuliwi over the counter? Yani, hazinunuliwi bila cheti cha daktari; na hasa kwa sababu, dawa za aina hii zinatumika na wale wenye uraibu wa dawa za kulevya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Katimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, haya ni mambo ambayo tunakuwa tunaelimisha. Katika elimu hii tunayoitoa ni kuhakikisha kwamba watu wetu hawafanyi hivyo. Ukimsikia Mbunge mwenzetu akisema kuna baadhi ya maduka ya dawa ambayo tumekuwa tunawafungia na wamekuwa wakipewa adhabu mbalimbali, ni kwa sababu ya makosa kama hayo na kuna utaratibu wa kusimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka kukuhakikishia tukienda sasahivi kuhakikisha kwamba maduka ambayo wafamasia waliopo wanaweka vyeti vyao badala ya kuweka cheti sasa wanaajiriwa wafamasia kwenye eneo husika, tutaondokana na matatizo kama hayo. Hii ni kwa sababu kwenye site atakuwepo mtaalamu wa dawa, atakuwepo na nesi ambaye ana utaalamu huo wa kuuza dawa na mambo mengine ambayo yatazuia hicho. Kwa sababu, hata kama ni duka la chini kabisa ni lazima anayeuza pale anajua dawa. Kwa hiyo, hayo matatizo yanadhibitika.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Kakonko – Kinonko – Guarama mpaka mpaka wa Muhange, ambayo ni barabara itakayounganisha Tanzania na Gitega, ambayo ni Makao Makuu mpya ya Burundi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Katimba, Mbunge Viti Maalum, Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya kuanzia Kakonko hadi Muhange ni kweli inaunganisha Tanzania na Burundi na sasa hivi Makao Makuu yao yamesogea Gitega. Ilikuwa haijafanyiwa usanifu, lakini tutakamilisha usanifu ikiwa ni maandalizi kwa kuijenga barabara hii yote kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu ya Serikali, aidha nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wahitimu wengi wa elimu ya juu wanategemea sana kuajiriwa tofauti na wahitimu wa kada ya kati ambao wanaweza kujiajiri wao wenyewe. Ukweli ni kwamba ajira hazitoshelezi kuajiri wahitimu wote.

Je, Serikali haioni haja ya kuwawezesha wanafunzi wa kada ya kati waweze kupatiwa mikopo ya kugharamia elimu yao kama vile wanavyopatiwa wanafunzi wa elimu ya juu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; Je, Serikali inamkakati gani wa kuboresha mitaala ya elimu ili kuweze kuwa na mafunzo ya msingi ya kuanzisha na kuendeleza biashara ili hawa wahitimu wa elimu ya juu watakapokosa ajira basi waweze kujiajiri wao wenyewe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Katimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye majibu ya msingi, upande wa utoaji wa mikopo nimesema kwamba Serikali inaendelea kujipanga lakini nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, wenzetu wa Benki ya NMB tayari imeshaanza utaratibu huo wa utoaji wa mikopo kwa upande wa elimu ya kati ambapo kwa mwaka huu wa fedha imeweza kutenga zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya utoaji wa mikopo, nasi kama Serikali tunaendelea na uratibu wa jambo hili ili tuweze kuangalia uwezekano wa kutoa mikopo hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwamba Serikali inatoa ruzuku ya kutosha kabisa kwa sababu kwenye vyuo vyetu vya kati wanafunzi hawa kila mwanafunzi mmoja anagharamiwa zaidi ya shilingi milioni moja kwa mwaka kwa ajili ya kusaidia vilevile na kupunguza gharama za ada.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili anataka kufahamu mikakati ya Serikali juu ya maboresho ya mitaala pamoja na sera. Nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge tunaendelea na utaratibu wa maboresho wa sera pamoja na mitaala, tumeshapata rasimu ya kwanza ya maboresho hayo na miongoni mwa maeneo ambayo tumeyatilia mkazo sana ni katika stadi za fedha pamoja na biashara ili wanafunzi wetu watakapotoka katika vyuo hivi aidha waweze kujiajiri au kuajiriwa.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika ahsante. Msingi wa kuanzishwa kwa mafunzo kwa vitendo kazini ni kuziba ombwe kati ya mafunzo waliyopata wahitimu vyuoni pamoja na soko la ajira. Sasa, kwa kutokuwa na kipaumbele cha kuajiri wale waliopata haya mafunzo kwa vitendo kazini kwanza, ni sawasawa na kupoteza lengo la kuanzishwa kwa mafunzo hayo. Sasa, kwa kutokuwa na kipaumbele cha kuajiri wale waliopata haya mafunzo kwa vitendo kazini kwanza, ni sawasawa na kupoteza lengo la kuanzishwa kwa mafunzo hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu swali la Mheshimiwa Zainab Katimba niruhusu kidogo na mimi nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

SPIKA: Mheshimiwa Ridhiwani huko ni kupoka madaraka sasa, endelea (Kicheko)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nisamehe kwa sababu niliona kwamba niombe ruhusa kwako, nadhani ujumbe umeshafika. (Kicheko)

SPIKA: Subiri na wewe umeweka historia, kwa hiyo, nimekuruhusu toa salamu zako. (Kicheko)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Zainab Katimba kuwa ni kweli anayoyasema Mheshimiwa Zainab Katimba na ndiyo maana nataka nikiri mbele ya Bunge lako, wakati wa mijadala mingi inayoendelea juu ya masuala mazima ya ajira na utumishi, jambo la mazoezi ya kujitolea au mafunzo ya vitendo limekuwa ni moja ya jambo la mjadala mkubwa.

Mheshimiwa Spika, Bunge lako limesema kwa sauti kubwa na Serikali imesikia. Ndiyo maana sasa tuko katika mchakato wa kufanya review ya Sheria yetu ya Utumishi wa Umma ili kuweza kuangalia mapungufu yote yaliyopo na kama nilivyosema kwenye ahadi yetu kwamba tutakapokuwa tayari tutaileta hapa na Bunge lako litapata nafasi ya kutoa mawazo na sisi kama Serikali tuweze sasa kutengeneza sheria ambayo itakuwa inabadilisha Sheria ya Utumishi wa Umma ili kuweza kutengeneza mustakabali mzima wa ajira na vipaumbele katika nchi yetu.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nina swali moja la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi wa umwagiliaji wa Bonde la Mto Ruichi uliopo Kigoma Mjini ili wanawake na wananchi wa Jimbo la Kigoma Mjini waweze kufaidika na kilimo cha kisasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Katimba, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Ruichi hivi sasa tumeshapata no objection kutoka Kuwait Fund na utaanza utekelezaji wake mwaka huu wa fedha 2022/2023.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, Serikali haioni haja ya kumjumuisha mtoto njiti kwenye Bima ya Mama yake ili pindi anapozaliwa aweze kupata huduma hiyo na kumwondolea Mama mwenye mtoto njiti adha ya kuanza kufanya usajili wa mtoto kwenye Bima ya Afya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, swali aliloliuliza Mbunge ni swali muhimu sana na nitumie fursa hii kumwagiza Mkurugenzi Mkuu wa Bima ya Afya kwamba suala la kuhudumia mtoto njiti ambaye mama yake ana bima yake ya afya lisiwe mjadala. Mtoto njiti akizaliwa na huduma yake inakuwa ni automatic. Vilevile kwa sababu tunakwenda kwenye suala la bima ya afya kwa watu wote Wabunge wote tukumbuke hayo mambo tuhakikishe sasa tutaweka kwenye sheria ijayo iweze kufanyika vizuri zaidi. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza. Je, Serikali ina mkakati gani wa kufanya ulezi kwa vikundi hivi si tu vya vijana lakini vikundi vya wanawake na watu wenye ulemavu, ili viweze kuwa na ufanisi katika kufanya shughuli zake za ujasiriamali?

Swali langu la pili, tathmini inaonesha kwamba malipo ya fedha hizi za mikopo zinazotoka kwenye Halmashauri bado zinasuasua. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba mikopo hii inalipwa kwa wakati ili waweze kunufaika vijana wanawake na watu wenye ulemavu wengi zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zainab Katimba Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati ambao Serikali imekuwa inaufanyiakazi katika kuhakikisha vikundi hivi ambavyo vinakopeshwa wajasiliamali wadogo wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kuwa endelevu lakini pia kuweza kuwa na tija ni Maafisa Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri husika kwanza kuwatembelea mara kwa mara, kuwafanyia mafunzo ya mara kwa mara, pia kuwashauri kuona kwamba wanakwenda vizuri na huo ndiyo ulezi wenyewe kwa maana ya kwamba viongozi wa Halmashauri lakini katika ngazi za Kata, Waheshimiwa Madiwani na Viongozi wengine wanahusika kuvifuatilia pia kuvishauri. Tutaendelea kufanya hivyo ili kuhakikisha kwamba vikundi hivi vinakopa lakini vinarejesha kwa tija.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na malipo ya fedha kusuasua ni kweli, kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya Watendaji kuchelewesha malipo haya na Serikali ilishatoa maelekezo kwamba kama kikundi kina kinakidhi vigezo kipate fedha mapema iwezekanavyo ili shughuli ziweze kuendelea, lakini mara nyingine zinacheleweshwa kutokana na baadhi ya vikundi kutokidhi vile vigezo vinavyotakiwa. Ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, Serikali haioni haja ya kumjumuisha mtoto njiti kwenye Bima ya Mama yake ili pindi anapozaliwa aweze kupata huduma hiyo na kumwondolea Mama mwenye mtoto njiti adha ya kuanza kufanya usajili wa mtoto kwenye Bima ya Afya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, swali aliloliuliza Mbunge ni swali muhimu sana na nitumie fursa hii kumwagiza Mkurugenzi Mkuu wa Bima ya Afya kwamba suala la kuhudumia mtoto njiti ambaye mama yake ana bima yake ya afya lisiwe mjadala. Mtoto njiti akizaliwa na huduma yake inakuwa ni automatic. Vilevile kwa sababu tunakwenda kwenye suala la bima ya afya kwa watu wote Wabunge wote tukumbuke hayo mambo tuhakikishe sasa tutaweka kwenye sheria ijayo iweze kufanyika vizuri zaidi. (Makofi)