Contributions by Hon. Tauhida Cassian Gallos Nyimbo (10 total)
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS NYIMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia toka Bunge hili lianze, nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchaguliwa na wananchi kwa kura nyingi. Pia nimpongeze Makamu wa Rais, Mheshimiwa Mama Samia kwa kuteuliwa, imani yetu wanawake hatatuangusha maana tuna uhakika na kazi anazozifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa wakati huu nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Dkt. Mohamed Ali Shein kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi na kwa imani yake na Wazanzibari. Nasema nampongeza Mheshimiwa Rais wa Zanzibar kwa sababu ameonesha hakika yeye ni kiongozi na kiongozi wa kupigiwa mfano. Uvumilivu wake, utu wake, ubinadamu wake umefanya leo Zanzibar iwe ni nchi ya amani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Rais huyu hakuwa kiongozi ambaye ni mchu wa madaraka, hakuwa kiongozi ambaye anashibisha tumbo lake, amekuwa kiongozi mwenye kuitakia wema Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Ukimya wake kwa muda wote na maneno yote kwa muda wote aliokaa kimya lengo lake lilikuwa ni moja kuhakikisha Zanzibar iko salama, kuhakikisha Tanzania iko salama. Kama Rais alikuwa na mamlaka tosha na alikuwa na kila cha kufanya na alikuwa na aina ya sababu ya yeye pia kujitangaza lakini hakufanya hivyo, alitaka kwenda kwa utaratibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii pia kumpongeza Waziri Mkuu kwa kuteuliwa kwake na kuthibitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Niwashukuru Mawaziri wote, imani yangu kwenu ni kwamba tutapiga hatua, hapa tulipo tutaendelea kusonga mbele. Tunaitegemea Tanzania mpya katika miaka mitano hii ijayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani zangu pia ziende kwa wapiga kura wangu ambao ni Wanawake wa UWT, Mkoa wa Magharibi. Nawashukuru kwa kunirudisha Bungeni na kuniamini kama mtoto wao naweza nikafanya kazi, nawaahidi sitowaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Spika, nikupongeze wewe kama mwanamke, ujasiri wako tumeuona na tumeona ukifanya kazi kama mwanamke ambaye hutuangushi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze moja kwa moja kwenye kuchangia. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri, kwa bajeti yake nzuri aliyoileta na nipongeze kikosi kizima cha Jeshi la Wananchi wa Watanzania. Kazi zenu ni nzuri zinaonekana ndiyo maana ukaona watu wanapiga kelele, mngekuwa hamfanyi kazi watu wangenyamaza kimya lakini kwa kuwa mnafanya kazi ndiyo maana watu wakapata fursa ya kunyanyua midomo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na wananchi wake kwa ujumla, niwapongeze kwa kumrudisha kila siku Bungeni kwa mbwembwe. Hii yote inaonesha ujasiri wake na uwezo wake wa kufanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sura ya tisa katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri imezungumzia suala zima la maendeleo ya viwanda, kilimo na ajira kwa ujumla. Vijana tumaini kubwa liko kwake. Akitaka kujua kama Tanzania vijana matumaini yako kwake aone wakati unapofika wa kuchukua watakaojiunga na JKT au jeshi kwa ujumla. Vijana wengi huhangaika na nafasi hizi kwa sababu matumaini yao kama vijana wa Tanzania yako kwake. Nadhani ni vema wakashirikiana na Wizara ya Viwanda na Kilimo wakaona ni jinsi gani wanaweza kuwasaidia vijana wa Tanzania. Naamini kwa kufanya hivyo tutaendelea zaidi kama vijana wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kwenye suala zima la uchaguzi. Toka tulipoanza Bunge hili hoja kubwa na michango ya Wizara zote zilizochangiwa ni hoja ya uchaguzi wa Zanzibar. Uchaguzi wa Zanzibar umekwisha, Rais yupo, anatawala, tunaendelea kama kawaida. Sasa hizi kelele unaenda kumpigia Jeshi la Wananchi wa Tanzania amekufanya nini? Kwa sababu wanaposema wanadhani hawana uwezo wa kuingia humu ndani ili kujibu. Jeshi la Wananchi wa Tanzania limeitendea haki Zanzibar. Kati ya vyombo ambavyo tunastahili kuvipongeza Tanzania ni pamoja na Jeshi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sikuwa na shida ya kuzungumza hapa, nazungumza kwa sababu jeshi hili halikumpiga mtu, halikumchapa mtu, halikumtukana mtu, halikufanya kitendo chochote cha kuweza kuzungumzwa kwenye Bunge hili. Jeshi lile limekaa Zanzibar kwa amani, limepita kwa mbwembwe, hivi jeshi linapita wewe unaogopa nini? Una masuala gani ya kukufanya uliogope Jeshi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania? Hebu tuambie hoja yako ya msingi juu ya Jeshi hili ni nini ili tuwapeni majibu ya uhakika. Toka Bunge lianze tumekosa jibu la kuwapa kwa sababu hatukuona suala la msingi juu ya masuala yenu mnayozungumza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi limekaa Zanzibar…
Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa nane wa kitabu cha hotuba ya Waziri wa Jeshi la Ulinzi kimezungumzia suala zima la kuimarisha muungano, mlidhani muungano unaimarishwaje? Mlidhani ile kuoa na kuoana tu kunatosha kuimarisha muungano? Muungano utaimarishwa na Jeshi la Ulinzi. Mimi niwapongeze, kati ya mtu ambaye anajisikia ufahari mkubwa leo kusimama hapa kuziona zile kofia zipo pale mmoja wao ni mimi. Tunawapenda, fanyeni kazi na kila uchaguzi ukifika msimsubiri Waziri awapeni amri. Jenerali upo, viongozi wote wapo tunataka mshuke iwe kwa boti, iwe kwa ndege na kadhalika lakini muingie Zanzibar kufanya kazi. Hata uchaguzi ukirudiwa warudi, wakitaka kuja kesho waje, kitakachotokea tunakuombeni mje msisubiri amri, fanyeni kama wajibu wenu, fanyeni kama kazi zenu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wamezungumzia mambo mengi kuhusu uchaguzi lakini tu tungependa kuwaambia kwamba uchaguzi pamoja na kwisha, kulikuwa na hoja zinazongumzwa na Tume, Mwenyekiti wa Tume alikaa kwenye TV zikachambuliwa kasoro, kila kitu kilichoonyeshwa kule, hamkuwa na hoja na ninyi kutafuta Kipindi mkajibu, mbona mlinyamaza kimya? Kama masuala mnayozungumzia kwamba document mnazo, mna ushahidi hata sisi document tunazo mpaka leo, kura mbili mbili zipo, saini wanaweka watu wawili wawili zipo, hakuna kilichokuwa hakipo! Mmebaki mnawinda lakini hayo mawindo yenyewe mnayowinda hakikisheni kwamba hayapo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa siku ya leo yangu yalikuwa hayo machache, nakushukuru kwa kunipa fursa hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii nami niweze kuchangia katika Wizara hizi mbili; Wizara ya TAMISEMI na Wizara ya Utawala Bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue fursa hii kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mheshimiwa Rais wetu ametukopesha Watanzania imani, ametukopesha Watanzania mapenzi, ametukopesha Watanzania utu wema, ametukopesha Watanzania kazi, ametutendea haki. Tunaahidi 2020 kulipa alichotukopesha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanamna pia ya pekee nichukue fursa hii nimshukuru Rais wangu wa Zanzibar,mwongeaji aliyepita kabla ya huyu aliyekaa alizungumzia Zanzibar naakasema kwamba hali ya kisiasa haiko vizuri. Niseme katika ukumbi huu kwamba Zanzibar hali ya kisiasa iko vizuri, Rais wa Zanzibar anaisimamia siasa ya Zanzibar vizuri hatuna mashaka usiku na mchana tunatembea bila wasiwasi na siasa inaendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze Mawaziri wa Wizara zote mbili nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Jafo, kazi kubwa anayoifanya pamoja na wasaidizi wake, lakini pia nimpongeze Waziri wa Utawala Bora kazi kubwa wanazozifanya Mwenyezi Mungu atawalipa, maana tukisema tu kwa mdomo haitoshi lakini tuseme kwa vitendo tunaiona kazi kubwa wanayoifanya, tunasimama kutimiza wajibu na kuona maeneo gani ambayo wanahitajika kuongeza nguvu ili tuweze kwenda vizuri kwa pamoja.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama leosuala kubwa ninalotaka kulizungumza ni suala la Mfuko wa Wanawake,Vijana na Watu Wenye Mahitaji Maalum. Nimwambie kaka yangu, Mheshimiwa Jafo pamoja na kazi kubwa na majukumu aliyokuwanayo na wasaidizi wake,aweke mkazo kwenye suala la Mfuko wa Vijana, Wanawake na Watu Wenye Mahitaji Maalum. Sehemu hii tunahitaji mkazo wa kipekee, suala kubwa ndani ya Taifa letu, janga kubwa tulililokuwa nalo ni suala la ajira kwa vijana. Kwa maneno ya vijana wanakwambia hatuna njia ya kutokea isipokuwa kwenye Mfuko huu. Kaka yangu, Mheshimiwa Jafo mengi anayoyafanya tunampongeza na mazuri, mazuri na yakupigiwa mfano. Tunamwomba kaka, kwa vijana wanawake na watu wenye mahitaji maalum aweke mkakati mahususi wa kuusimamia Mfuko huu ambao utakwenda kuwakomboa wanawake na vijana. Mfuko huu upo na unafanya kazi, lakini unasuasua, haupo vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa ndani ya Kamati ya LAAC miaka mitano Mwenyezi Mungu aliyonipa kibali cha kuingia Bungeni kupitia nafasi za vijana, nilikaa ndani ya Kamati ya LAAC, Mfuko huu haufiki kwa vijana kama ipasavyo, haufiki kwa wanawake kama ipasavyo na kwa sasa tumeongeza kufika kwa watu wenye mahitaji maalumu. Mpaka sasa ninavyoongea namshukuru Mheshimiwa Spika kwa kunirudisha tena kwenye Kamati ya LAAC, kwahiyo napata kujua tathmini mambo yanakwendaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jafo halmashauri zinaendelea vizuri,hatusemi kwa asilimia mia moja, lakini zinaendelea vizuri, jitihada zake zinafanya kazi, aweke mkazo kwenye Mfuko huu ili vijana wapate kutoka, akiwapa fursa vijana kutoka kupitia Mfuko huu, namwambia kaka, Mheshimiwa Jafo hatuna wasiwasi na yeye, Mwenyezi Mungu aendelee kumbariki maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti,Mfuko huu waVijana, Wanawake na Watu Wenye Mahitaji Maalum ndiyo kwenye kilio, labda kaka, Mheshimiwa Jafo ifike wakati nikutolee mfano, kuna halmashauri ya mwisho wakati tupo kwenye Kamati, tulikwenda Halmashauri ya Kahama kama sikosei. Halmashauri ya Kahama wana mradi unahitwa unaitwa Mradi wa Dodoma. Kaka, Mheshimiwa Jafo mradi ule umetoa ajira kupitia huo huo Mfuko, ajira elfu moja mia tano na sabini na tisa, lakini hapo hapo wamepatiwa viwanja wanawake, vijana na watu wenye ulemavu watu738.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama nimwombe jambo moja tu kaka, Mheshimiwa Jafo, aendeakakague kama itamridhisha, kama ule mradi umefanywa upo sana salama ashawishi na halmashauri nyingine ziige. Ni mfano wa kuigwa, leo kijana wa Tanzania aliyekuwa akiuza karanga, aliyekuwa akipanga mananasi matatu, manne, Serikali hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli Rais wetu anapata hati miliki ya kiwanja bure.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kamakaka, Mheshimiwa Jafo utamridhisha,atauhisi uko salama, hautakuwa na matatizo mbele ya safari akauangalie,ashawishi na halmashauri nyingine. Naamini kama utakuwa mradi mzuri, basi halmashauri nyingi zikitaka, vijana watapata mabadiliko kwa sababu leo kijana ana hati miliki kwamba ana sehemu anapamiliki, anaenda kukopa wakati wowote, saa yoyote, benki yoyote, kwa sababu hati miliki ya kumiliki anayo.
Sasa nimshauri na kumwomba Mheshimiwa Jafo kwamba, akiangalia na ukimridhisha, kama itawezekana mfumo unaotolewa fedha kwa vijana kupitia halmashauri, kwa sasa fedha hazina marejesho, vijana wakipewa fedha hawarejeshi, lakini kama tutatumia mfumo huo kwamba amepatiwa viwanja bure,wameenda kukopa huko mwenyewe, wataelekezwa utaratibu mzuri wa kukopa, watasimamiwa na mabenki basi mambo yataendelea kwenda vizuri.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimwambie kaka, Mheshimiwa Jafo kwamba tuwapongeze pamoja na Utawala Bora, zamani ukienda halmashauri, wafanyakazi wa halmashauri, Mkurugenzi kaenda leo wanasema kesho ataondoka, lakini sasa hivi mambo hayako hivyo, kila mfanyakazi aliyekuwepo kwenye halmashauri akiiona Kamati ya LAAC anatamani kuulizwa ajibu nini kinaonesha kwamba wafanyakazi wameelimika, wamefundishwa vya kutosha, utawala bora unaonekana. Niwaombe kwamba waendelee kusimamia bila wasiwasi…
T A A R I F A
MWENYEKITI: Taarifa Mwakanyoka.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa mzungumzaji, amekuwa ana tamka mara kwa mara kaka Jafo kwa mujibu wa kanuni, ni kwamba lazima aheshimu sana nafasi yake awataje kwa vyeo vyao kama ni Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI aseme ili na watu wamwelewe na hansard ziweze kusoma vizuri. Ahsante sana. (Makofi)
MWENYEKITI: Mheshimiwa Tauhida.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti,naipokea taarifa yake. Asiwe muungwana kwa hapa, awe muungwana na kwa mengine wanayoyaona Rais yetu anayoyafanya na Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakiri ni Mawaziri, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI naomba waendelee kuwasimamia wafanyakazi. Kulikuwa na tatizo sugu la mfanyakazi anaharibu halmashauri moja, ugonjwa wake unahamishiwa halmashauri ya pili, kaka Jafo…
WABUNGE FULANI: Aaa,aaa. (Makofi/Kicheko)
MHE. TAUHIDA CASSSIAN GALOSS NYIMBO: Mheshimiwa Waziri sijaona kipindi hiki hilo tatizo, hilo tatizo limepungua kwa asilimia kubwa. Niseme kwamba kulikuwa na matatizo ya ma-engineer kutokujua wajibu wao, lakini sasa mambo yamebadilika hayajaondoka, hayajamalizika, lakini yamepungua. Kwahiyo, Mheshimiwa Waziri kwa maeneo wanayofanya vizuri lazima tumpongeze, lakini asiache kuendelea kusimamia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo pia la kukaimu, Mheshimiwa Waziri ajitahidi kwenye hili. Mtendaji waHalmashauri unapomwambia kakaimu hawajibiki ipasavyo, kwanza anawajibika kwa hofu, jambo la pili anachofanya ni kufanya kazi kwa kutokujiamini. Kwahiyo, Mheshimiwa Waziri kamahili eneo utalisimamia kumaliza suala la watu wanaokaimu, litatusaidia na tutaendelea kufanya kazi vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine linalosumbua ni suala la Wanasheria waliokuwepo ndani ya Halmashauri. Nafikiri ni muda mzuri wa kukaa na Wanasheria waliokuwemo ndani ya halmashauri na wanaotaka kuwapeleka, kwa sababu baadhi ya halmashauri bado hazina Wanasheria, mambo mengi ambayo yanaharibika ndani ya halmashauri chanzo kinachosababisha na kinachochangia pia ni kutokuwa na Wanasheria wazuri. Wapeleke Wanasheria wazuri ambao wataweza kuisaidia halmashauri hususan kwenye suala la kuingia mikataba, halmashauri zimekuwa zikilega lega au zikiharibika kwenye suala hili au haliko vizuri. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri kama maeneo haya atayakazia vizuri na kuyasimamia vizuri, nafikiri kwamba kero na matatizo ya ndani ya halmashauri yatakwisha.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Tauhida.
MHE. TAUHIDA CASSSIAN GALOSS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwaasilimia mia moja.(Makofi)
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimshukuru Waziri Mheshimiwa Ummy Mwalimu pamoja na Naibu wake Waziri Dkt. Kigwangalla, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya ndani ya Wizara hii. Pia nimpongeze Rais wangu aliyetokana na Chama cha Mapinduzi Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri na kubwa anayoifanya katika Taifa hili la Tanzania. Wananchi wa Tanzania tuna furaha kwa kazi kubwa ambayo anaifanya na kuwatendea haki Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ni kubwa, Dada yangu Ummy Wizara ni kubwa, kazi na majukumu uliyokuwa nayo ni makubwa, lakini haina budi ukiwa kama mwanamke mwenzangu nikupongeze kwa ufanisi mkubwa wa kazi na uwezo uliokuwa nao wa kazi, kuweza kumudu Wizara hii kubwa na Wizara ambayo imebeba watu wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumza watu wote, majigambo ya Wabunge, majigambo ya Makatibu Wakuu, majigambo ya waendesha boda boda yote yanategemea afya zao na umezibeba wewe dada yetu Ummy pamoja na kaka Kigwangalla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nisiache pia kuzungumza suala zima la afya kwa watoto. Mheshimiwa Waziri umelizungumza katika kitabu chako, umelizungumza na kuliongea kwa kina suala zima la afya ya watoto katika ukurasa wa tano, umelizungumza na umelitendea haki, ila dada yangu nikuombe ukiwa kama mwanamke kumbuka unapokwenda labour unapofikwa na uchungu. Unayoyafanya yote ni mazuri lakini wajibu wetu kukukumbusha kuna baadhi ya maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatupaswi kulaumu, tunapaswa kukuambia ili ukumbuke na kuangalia maeneo mengine. Unapokwenda labour mwanamke unaujua uchungu na dada yangu Ummy una watoto uchungu unauelewa. Watoto wamefikwa na janga kubwa linalowasumbua sasa la kubakwa, hatuna budi kama mwanamke angalia kwa jinsi ya pekee tatizo hili tunalitatuaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalizungumza Dada Ummy huwezi kulitatua peke yako, lazima kuna baadhi ya watu mshirikiane au Wizara mshirikiane. Lazima ushirikiane na Wizara ya Mambo ya Ndani, lazima ushirikiane na Wizara ya Katiba na Sheria. Dada Ummy ni nafasi yako kama mwanamke kaa nazo Wizara hizi muone tatizo hili mnalitatuaje. Leo kilio cha kila mwanamke ndani ya Nchi hii, ubakaji wa watoto na unyanyasaji wa watoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna njia nyingi za unyanyasaji wa watoto, lakini kwa sasa yenye sura ya pekee ndani ya Tanzania ni suala la ubakaji. Nimeambiwa jana Dada yangu Faida amesimama mpaka amefikia kulia, suala la ubakaji ni suala kubwa, Dada Ummy unafanya kazi kubwa lakini kaa na Wizara zingine hutalitatua peke yako na kulimaliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalizungumza hivi kwa sababu, Wizara hizi imefika wakati unapokwenda Mahakamani unaambiwa limekwama Wizara ya Mambo ya Ndani kwa maana polisi, lakini polisi ukifika ukifuatilia unaambiwa limekwama hatuna maelezo ya kutosha ndani ya Wizara ya Afya. Tulione suala hili linakwendaje na suala hili Dada Ummy linahitaji pia elimu ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake wenzetu wengine hawafahamu kwamba mtoto unapompeleka ukamtia maji, tayari baadhi ya uthibitisho unaufuta kabisa. Inapaswa lazima kama mwanamke usimame na kutoa elimu ya kutosha ili tuone tatizo hili kama Serikali na kama viongozi tukiwa tuna nia moja na lengo moja ya kulitatua tatizo hili limalizike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 26, ulizungumza kwa makini na kwa kuitolea maelezo ya kutosha hospitali ya Muhimbili. Ndani ya mwezi mmoja uliokwisha nilikuwepo Muhimbili kwa muda wa siku tatu, ilinibidi nikae pale. Panapostahili sifa binadamu apewe sifa. Mmefanya kazi kubwa lakini naamini kazi hii anayewatia nguvu na kukuwezesheni ni Mheshimiwa Rais. Inapofika wakati kama viongozi tusiwe wingi wa kulaumu tukakosa kushukuru. Unapoizungumzia hospitali ya Muhimbili uwe umekwenda umefika. Kuna tofauti kubwa ya nyuma tulipotoka na sasa hivi, lakini kwa sababu kuna baadhi ya watu nilipoenda, nilifanya kazi nikiwaona nisiache kuwataja kwa majina, lazima niwasifie. Kiongozi unapopata muda, posho tunayowalipa haitoshi kwa madaktari lakini basi...(Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kuunga mkono hoja, ingawa nimeambiwa nina dakika kumi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii kwa kuchangia Wizara ya Elimu. Kwanza kabisa nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi kubwa na jitihada yao wanayoifanya, kwa kweli sisi kama Watanzania tunaiona wenyewe kwa macho. Kinachonifurahisha na kuniridhisha zaidi ni kwamba Mawaziri wote wawili ni wanawake. Mara nyingi wanapofanya kazi wanawake mimi kama Tauhida huwa najisikia ufahari mkubwa lakini hatuachi kusema mambo madogo madogo ili waweze kuyafanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mimba kwa watoto wa kike linahitaji umakini kwenye kutoa uamuzi. Ukiangalia suala hili kwa pande zote mbili kwa hoja zinazojengwa basi kila mmoja ana tafsiri yake. Naamini kwamba Waheshimiwa Wabunge ni watu makini na watatoa maamuzi sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye ukurasa wa 28 na 29 wa Taarifa ya Kamati, kuna sheria zinazomhusu mtoto wa kike, naomba ziangaliwe na zifanyiwe kazi. Nasema zifanyiwe kazi kwa sababu sheria ambayo ilitakiwa iletwe ni anayempa mimba mtoto wa kike kuwekwa ndani. Imani yangu ni kwamba atakayempa mimba mtoto wa kike akiwekwa ndani nina uhakika kwamba suala la mimba kwa wanafunzi litakoma au suala la mimba kwa watoto wa kike litakoma kwa sababu mtiaji mimba ataogopa kuwekwa ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme kwamba ifike wakati kama wananchi na Watanzania tukubaliane kwamba mtoto wa kike anatakiwa apewe elimu ya kutosha, tusiwe watu wa kufumba maneno. Suala la kufumba maneno ndiyo limetufikisha hapa leo kutokubaliana.
TAARIFA...
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Mchengerwa kwa ufafanuzi na maelezo mazuri, nayakubali kwa kuwa mwanasheria ametoa jambo la ziada zaidi kutukumbusha, naikubali taarifa yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri Mheshimiwa Waziri amesikia kwa sehemu, naomba aweke mkazo kwenye maeneo hayo, yeye ni mama, ni mwanamke, hatupendi kuwa na Taifa wanawake wakakosa fursa ya kufanya kazi, kwa sababu tu ya hali ambayo wao hawakupendezewa nayo na wala hawakukubaliana nayo. Umri mtoto anaopata mimba ni mdogo, anarubuniwa, nafikiri ni wakati wa kulishawishi Bunge hususan wanawake wenzangu tuliotoka kwenye Viti Maalum kwamba tuje na mikakati ya makusudi na sheria za makusudi, mtoto mwanamke atafutiwe jinsi ya kulindwa aendelee na masomo yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiamue kwa utashi tu, tusifikie wakati tukaamua bila kujua nini athari yake mbele. Ningeridhia sana kama ingekuwa bakora hii na sisi tuliokuwemo ndani ingetukamata. Nazungumza kama ingetukamata kwa sababu watoto wengi wanaothiriwa na hili ni watoto wa vijijini, watoto wa kimaskini. Nazungumza hivi Mheshimiwa Waziri kwa kuwa tunaishi mitaani tunaelewa nini kinachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mtoto yeyote wa mtu aliyepo humu ndani, tena namshangaa baba yeyote anayesimama humu ndani akadhani kwamba hakielewi kinachoendelea kule nje. Mtoto anayepata fursa ya kusoma ni mtoto wa mwenye pesa, ndio anayepata fursa ya kusoma, tufikie wakati tuwafikirie na walioko chini. Nazungumza mtoto yoyote wa mwenye pesa akishika ujauzito, ikifika mwezi mmoja au miwili anaenda kutolewa mimba kimya kimya inapita, baba ndani ya nyumba yake haelewi mtoto wake kama katolewa mimba maana haugui lakini isitoshe mtoto huyo huyo atatafutiwa shule ya mbadala kwenda kusoma. Inaniwia vigumu kutokuitendea nafsi yangu haki, nataka apewe fursa mtoto wa kike kuendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, kwangu mimi ni kigezo Wabunge wangapi wa kike humu mnaendelea kusoma. Wabunge mmebeba mimba zaidi ya tano ya sita mmezaa na mnakaa na waume zenu. Tuwatafutie mustakabali watoto wa kike tunawafanyaje, tunawasaidiaje? Huwezi kuwa Mbunge wa Viti Maalum uliyeteuliwa na wanawake wenzio… (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuchangia. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Rais wangu wa Zanzibar kwa kazi kubwa anayoifanya kwa kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar katika sekta mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue fursa hii nimpongeze Makamu wa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya hususani wakati huu amejikita kwenye suala la mazingira pamoja na Wizara yake, kazi inafanyika vizuri. Matumaini yangu kwamba baada ya hapo mtaendelea kuondosha kero ndogo ndogo za Muungano zilizobaki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa jinsi ya pekee nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nampongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi na vitendo vikubwa na mambo mengi anayowafanyia Watanzania yenye tija, yenye muonekano na yenye faida kwa wananchi wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue fursa hii kumshukuru Waziri na Naibu wake kwa kitabu chao kizuri, chenye mwelekeo na mwonekano wa kutatua kero za Muungano hususani pale kaka yangu Mheshimiwa January alipomalizia kusema yupo tayari kupokea kasoro ndogo ndogo na kero ndogo ndogo za Muungano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa jinsi hiyo basi nafarijika kumwambia kwamba kero ndogo ndogo za Muungano zipo na kweli zinahitaji utatuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kwenda moja kwa moja kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa tisa ambapo amezungumzia suala la elimu juu ya la Muungano.
Mheshimiwa Waziri na Naibu wako suala la elimu kwa Muungano linahitajika na siyo kuhitajika nje tu kwa wananchi hata Bungeni kwa Wabunge sisi tuliokuwepo humu tunahitaji kujua faida za Muungano, tunahitaji kujua uwepo wa Muungano na tunahitaji kujua nini maana ya Muungano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwambia kaka yangu Waziri inawezekana ukachukua muda mkubwa kuwaelimisha wananchi lakini wenyewe Wabunge hatukuelimika juu ya suala la muungano. Maana leo ukisimama Mbunge unazungumza suala la Muungano kana kwamba sio Mbunge inakuwa haina afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili kwangu ni ombi kwa Waziri naomba suala la elimu ya Muungano tupewe na sisi Wabunge, inawezekana Tauhida ninavyouangalia sivyo anavyouangalia mwingine. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri niombe elimu hii atakapopata fursa atuletee Bungeni ili tunapotoa michango kama Wabunge tujue nini tunazungumza juu ya suala la Muungano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kati ya hivyo vitu vidogo vilivyopo. Kaka yangu Mheshimiwa January anakuja kila siku Zanzibar na tunamwona, sasa hivi hata mtoto wa miaka mitatu anamjua. Tunachokiomba kwake sasa atumie boti aache kutumia ndege, atumie boti kwenda Zanzibar ili apate kuona kero za wananchi wanyonge, mnyonge hapandi ndege, mnyonge siku zote anapanda boti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwambia kaka yangu Mheshimiwa January kwa sababu akipanda boti atajua nini kinachowakabili wananchi wa Tanzania katika suala zima la Muungano. Leo kaka Mheshimiwa January kijana kuliko yeye, umri chini yake, anatoka Zanzibar kwenye sherehe za pasaka Mtanzania bara anabeba TV ya inchi 14 kafurahia pasaka anasema nakuja huku nipate hii TV ya inchi 14, anatozwa ushuru ambao hatuufahamu mpaka leo. TV kainunua 125,000 anaambiwa TV ile ilipiwe 100,000, kijana kwa jicho langu namwona anaipiga chini TV bandarini vitu ambavyo ni vya masikitiko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wakati anazindua mradi wa reli…
T A A R I F A . . .
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa kaka yangu January zinapoongelewa kero achukulie mfano wa ndoa ya mtu mwingine yoyote, maana hata kero kwenye ndoa zetu huwa haziishi. Kwa hiyo, Mheshimiwa January hizi ni changamoto aziandike aone jinsi gani ataweza kuwasaidia Watanzania. Leo kijana anakwenda pale anaipiga TV , amini Mungu kuna baba amebeba viporo vitupu zaidi ya ishirini anaenda kutia dagaa anatoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar vitupu, anachajiwa kiporo kimoja kanunua shilingi 100 anaambiwa alipe elfu 50, gharama ya vipolo vile 20,000. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama nimwambie Mheshimiwa kaka yangu January, Rais alizungumza wakati anazindua mradi wa reli, alisema kuna watu wana hujumu Taifa hili kwa kusingizia Muungano, kwa kutupia tope Muungano na wanatumwa na baadhi ya viongozi wenzetu. Mheshimiwa January kaka yangu, naomba kama kuna watu tusimsubiri kila kitu afanye Rais, aende, apite bandarini, tukisema hili Mheshimiwa kaka yangu atoke Makamu wa Rais aende litatia aibu, atoke, aende, akaangalie nini kinachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo unawatoza wananchi kodi? Hiki kinafanywa kaka yangu sio lengo la Serikali, baadhi yao hawajaagizwa na Serikali, wanafanya kusudi kuupaka tope Muungano wetu. Kaka amepewa dhamana kubwa, dhamana aliyopewa Rais alijua ataitendea haki nchi hii, atawasaidiaje Watanzania, atumike kwenye nafasi yake, atoke, aende kama kuna viongozi au watendaji anahisi ni wabovu awatoe, afute. Rais amewazungumza sio mara moja, mara mbili wala mara tatu, Rais kila siku anawakemea lakini hivi vilivyobaki vifaurongo ahakikishe anaviondosha yeye, hatuhitaji Rais aende akamalize kazi ile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwambia Mheshimiwa kaka yangu January leo kero iliyopo pale kwenye Muungano ndio tutazimaliza hapa, kuna kero kubwa. Unakuta mtoto anatoka shule hii Tanzania ni yetu, anatoka shule Tanzania Bara labda anasoma Morogoro, anakwenda zake Zanzibar, tumezoea tiketi ni Sh.25,000/= anafika pale mwanafunzi wa shule anaambiwa akate tiketi ya Sh.50,000/= au Sh.60,000/=.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatukatai kuna biashara za watu binafsi tunajua hakuna uhuru usiokuwa na mipaka, uhuru wowote una mipaka. Ikiwa nchi watu wanataka kufanya kazi bila kuwa na mipaka hatutokwenda, lazima kama kuna wafanyabishara binafsi washughulike nao, wazungumze nao. Huwezi kumchukua mtoto wa miaka 15,12 au 13 kavaa sare zake za shule na begi yake anatoka shule likizo, simu haruhusiwi kwenda nayo shule, mzee wake kamtumia pesa kupanda boti ya Sh.20,000/=... (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa jioni hii kuweza kuchangia Wizara hii ya Habari na Michezo. Kwanza kabisa nichukue fursa hii ya kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake lakini kwa umuhimu mkubwa nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri, naamini kwamba anafahamu na anaelewa kwamba yeye ni baba na baba siku zote kazi yake ni kulea, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri nichukue fursa hii kumshukuru kwa sababu anajua kwamba ni wajibu wake kulea. Wizara alionayo takribani vijana wengi wa Tanzania wapo hapo. Vijana wa Tanzania shughuli kubwa wanazozifanya kwa sasa wamekimbilia kwenye suala la sanaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajielekeza zaidi kwenye vijana nizungumzie chombo chetu cha TBC. Chombo cha TBC kiumri mimi siwezi kuipata lakini inafikia wakati inatubidi tuizungumze na nategemea kwamba kuna baadhi ya Viongozi wa TBC watakuwepo mahali hapa. Kwa kweli mfumo wao wa kazi wengine hauturidhishi na maeneo hususan yasiyoturidhisha TBC ni pale ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri wanapokuwa na mambo mahsusi kwenye taarifa za habari niliwahi kuzungumza miaka mitano nyuma iliyopita, lakini sidhani hili kama nina hoja ya msingi kuishawishi Serikali yangu iwaongezee bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi suala la kukaa la kupanga vipindi vipi wafanye, hili linahitaji bajeti gani kwa sababu mimi ninavyofikiria, nadhani kwamba ni suala la karatasi na peni na kukaa na Watendaji Wataalam wakajipanga. Sidhani hili kwamba linanishawishi kuishawishi Serikali kwamba waongeze fedha ili kuweza kulifanikisha hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu ni jambo la aibu, tena ni aibu kweli kukuta chombo kama cha TBC tunachokitegemea wanafanana na vyombo vingine vya habari ambavyo vinamilikiwa na watu binafsi au wao kupitwa na vyombo vya watu binafsi. Hivi leo TBC Rais amekwenda kufungua miradi tofauti na mikubwa, kweli kwenye taarifa ya habari unachukua dakika tatu, anasimama Mheshimiwa Tauhida leo kaenda Jimboni kwake dakika tatu, akisimama sijui nani dakika tatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais ni Rais wa nchi hii tuwape fursa viongozi wetu hususan Rais wetu, apewe fursa na hakuna chombo kinachoweza kumpa fursa zaidi ya TBC. TBC wametutia aibu, chombo chao tulitegemea ndiyo kiwe mkombozi wa Watanzania kwenye kutoa habari, hivi leo TBC nikwambieni ukweli, hivi kweli leo Wabunge tukasimame hapa tukaisifie ITV, Azam tena na Wasafi TV sasa wanaikimbiza TBC, kitu ambacho kwangu ni aibu najisikia vibaya kusimama hapa kuizungumza TBC. Hamu yangu na shauku na niliwahi kuzungumza kwenye Bunge, siyo vibaya ku-copy kwa ndugu yako. Leo Zanzibar wanaweka vipindi wanaweka mpangilio wa TV kujua sasa taarifa ya Rais inatoka kwenye chombo cha habari. Leo unakuta watu wanakimbia wanaenda kuwahi kufungua taarifa ya habari anafungua TBC, baada ya dakika tatu anaona sherehe ya harusi ya mfanyakazi wa TBC.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Azam, mmoja wao niliangalia katika shughuli ya Ali Kiba niliangalia, walifanya vizuri walijua muda wa kutenga kuweka shughuli ile. Leo TBC tunategemea waweke vipindi vyao vizuri wapange mpangilio kwa itifaki kwamba inakuja ripoti ya Rais, inakuja ya Makamu wa Rais, inakuja Waziri Mkuu tunakwenda kwa itifaki hii, nchi inaongozwa na itifaki. Huwezi kumpangia Rais anazungumza kwenye taarifa habari dakika tatu au dakika nne siyo kitu kizuri, TBC kwa hili naomba wabadilike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri alichukue, nililizungumza miaka mitano nyuma imepita, naomba alichukue alifanyie kazi. Hivi hili niliombee bajeti gani, liongezwe bajeti gani, hivi Rais anaongelea masuala ya ndege, anaongelea masuala ya Tanzania kwenye miradi ya reli, anaongelea wananchi jinsi gani wanaweza kunufaika na mazao yao, anapewa dakika tatu kwenye taarifa ya habari na hizo TV nyingine zinafanyaje? Naomba Mheshimiwa Waziri walifanyie marekebisho hili. Bajeti ijayo nafikiri nitakuwa namba moja kukamata shilingi ya mshahara wa Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri tuje kwenye suala la sanaa, kwa wasanii limekuwa sawa na ng’ombe wa nyuma kutandikwa bakora, wakati ngombe wa mbele hatembei. Kwa kweli, Mheshimiwa Waziri inatubidi tuseme, atusamehe watoto wake, wasanii wanaonewa, tufike wakati tuseme wanaonewa. Hii BASATA inafanya kazi gani? BASATA kabla ya nyimbo ya msanii kutoka wao ndiyo wanaotakiwa kujua anaimba nini, kwa sababu kwenye Kiswahili kuna kitu kinaitwa tungo tata. Sasa inawezekana wasanii kuna maeneo wanatumia tungo tata, kama wanatumia tungo tata Baraza lipo, wanafanya kazi gani? Mheshimiwa Waziri hebu atupe mfano hii BASATA hebu awatoe, wanachokifanya wanawaonea wasanii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani wapewe posho, mishahara, kazi wanayotakiwa kuifanya hawaifanyi matokeo yake msanii ameshajituma, ndani ya mwaka mmoja ndio anakuja kufungiwa nyimbo yake. Hatumaanishi kwamba kila kinachofanyika ni kizuri hapana, nyimbo inawezekana ikawa mbaya na inawezekana maneno yaliyotumika yakawa mabaya na wanavyofanya baadhi ya wasanii na sisi haturidhiki navyo, lakini kuna chombo kinatakiwa na wao wawajibishwe ili twende sawa. Asipigwe bakora ngombe wa nyuma wakati wa mbele hatembei. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie vilevile kitu ambacho dada yangu Devotha hapa alizungumzia, Waziri aje na sheria, aje na kanuni kila kinachohusu sheria kama kuna sheria zimekaa upande huko atuletee maana Mheshimiwa Devotha anavyozungumza kazungumza kwa kujua anakizungumza nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza hili kwa sababu sheria lazima zije Bungeni tuziweke sawa. Haiwezekani Mmiliki wa Vyombo vya Habari akaamua kufanya anachokitaka yeye mwenyewe kisa tu kwamba wana uhuru, uhuru usiokuwa na mipaka una tatizo. Uhuru wowote anaopewa binadamu ukiwa hauna mipaka unakuwa na matatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo utamkuta mmiliki wa chombo binafsi kakorofishana tu. Nimtolee mfano Ali Kiba samahani kama italeta shida. Leo anaenda kuimba kakosana na mmiliki wa vyombo anafunga hata nyimbo zake kutokuimba, sidhani kama ina tija, sidhani kama ina faida. Sasa hizi sheria anazozizungumza dada yangu zije Bungeni hii ni nchi inaongozwa na watu makini. Sheria Waziri alete Bungeni tuzifanyie kazi lazima watu wote tufuate sheria twende na utaratibu, siyo kila mtu aamue anavyotaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue fursa hii ya kuwapongeza wasanii wengi wanaofanya vizuri kuliwakilisha Taifa letu. Kwa siku ya leo nimpongeze dada yangu Monalisa amefanya vizuri, amevaa bendera ya Tanzania na picha zake zote ukiziona nyingi takribani ana bendera ya Tanzania. Siyo yeye tu na wengi wapo wanaofanya kwa ajili ya kutetea Tanzania. Hili linaonesha sura fika kwamba sanaa ni faida kwetu, sanaa ina uwezo wa kuongeza kipato kwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee kidogo Waziri atakapokuja kufanya majumuisho siyo mtaalam sana kwenye mambo ya michezo, lakini kipindi cha nyuma tulikuwa Zanzibar sana tunalalamikia masuala ya michezo ila kwa sasa shwari imepatikana...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuchangia Wizara ya Elimu. Kwanza kabisa, nachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi kubwa wanazozifanya. Tunawapongeza, jitihada zinaonekana wanafanya kazi vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri na kikosi chake chote anachofanya kazi tunawapongeza; na kama Watanzania hatuna la kuwaambia zaidi ya kuwaambia waendelee kufanya kazi. Sisi tunasimama, ni wajibu wetu kuangalia maeneo gani tunaweza kuboresha ili tujenge Tanzania kwa nia moja na kwa nia ya kuleta maendeleo kwa wananchi wa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ametumia muda wake vizuri na muda mwingi kuboresha elimu ya juu na ameitendea haki. Michango ya Waheshimiwa Wabunge itaendelea kuboresha katika malengo yake na misimamo yake ya kutaka Tanzania iwe na elimu bora na yenye malengo na yenye ufanisi. Ndiyo maana halisi ya michango inayotoka ndani ya Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri achukue fursa kwa muda uliobaki. Tukiwa kama Wabunge wenzake tuungane kwa pamoja tuboreshe elimu ya msingi. Muda uliokuwepo kwa sasa, autumie kuboresha elimu ya msingi. Ametumia muda ipasavyo kuboresha elimu ya juu, sasa tunataka kuboresha elimu ya msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwa wakati huu, kati ya vitu ambayo vinapaswa kuboreshwa katika elimu ya msingi ni pamoja na kupeleka walimu wa kutosha ndani ya shule. Katika elimu ya msingi tunahitaji walimu wa kutosha. Mheshimiwa Waziri aweke mikakati, ashirikiane na Mawaziri wenzake kuona wanashusha walimu ili wawe kuwapatia elimu ya msingi ya kutosha wanafunzi wa shule za msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Waziri kwa masikitiko kabisa, nilikuta shule moja, nakumbuka Liwale; nimebahatika kutembea Liwale kijiji kwa kijiji, nilikuta shule ina Mwalimu Mkuu na Mwalimu mmoja, lakini kuna watoto vijana wa form four na form six, wakaamua kujitolea kuwasomesha wanafunzi wa kijijini kwao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna watu wanaamua kujitolea ndani ya vijiji vyao, maeneo wanayotoka, kufanya kazi kwa uzalendo, kwa nini tusiwape kipaumbele na fursa ya ajira?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kijana anakaa Kigoma unamshawishi kukumwondoa Kigoma kumpeleka Liwale, mazingira anayokumbana nayo huwa magumu. Ndiyo maana kelele kubwa za Wabunge kutokuwepo walimu wa shule kusomesha, hususan kwenye elimu ya msingi. Walimu wanakimbia kwa sababu ya mazingira wanayokumbana nayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimchukua anayetoka kijiji kile kile, hata suala la kukaa na makaazi kwake inakuwa rahisi. Kama hakukumbana na familia yake akaishi, basi atakuwa ana mategemeo ya pale anapoishi. Namwomba Mheshimiwa Waziri kwenye suala la walimu aweke mkakati na mkakati wake kwa uwe kipindi hiki cha Bunge tulichokuwanacho, mwaka mmoja na nusu ili tuweze kumalizia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama hapa ikiwa ni mara ya pili nikiongelea suala la Wizara ya Elimu. Kati ya kero kubwa ambayo naona inaitendea dhambi nafsi yangu, kuwepo shule na bar ikawepo karibu. Nimeshaizungumza Bungeni, kwangu kimekuwa kilio kikubwa. Haiwezekani tuwe na shule na Bar iko pembeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kama Watanzania tunategemea nini? Shule na Bar ipo pembeni; tuna mikakati gani kwa wanafunzi wetu? Tena unakuta ni shule za watoto wa primary, tunategemea nini Mheshimiwa Waziri? Hili nililiomba niliwahi kulizunguza. Hili halihitaji bajeti. Linahitaji tamko. Lazima tujue. Haiwezekani ijengewe na Bar hapo hapo. Tunawafundisha nini watoto wetu? Leo mtoto akitaka kununua soda, anakwenda Bar, akitaka maji anakwenda Bar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichonifanya nisimame kuongea, watoto wanafanya mitihani ya darasa la saba wote wanachungulia nje muziki unapigwa usiku. Hatuwatendei haki Watanzania. Ninalizungumza mara ya pili nikiwa Bungeni. Mheshimiwa Waziri toa tamko, wenye Bar waondoke kwenye shule, tunataka tuwatengeneze mikakati wananchi wa Tanzania na wananchi wa Tanzania. Anayejenga Bar kama mwenda wazimu tunamwambia aondoe Bar katika shule, hatutaki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine niliokuwa nalo, natamani sana kuona tunaambukiza uzalendo wananchi wa Tanzania, tuanze kuwawekea uzalendo kwenye utoto wao. Yaani tukimplekea mtoto wa shule wa primary kumpeleea uzalendo tunatakuwa na nchi nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uzalendo uanze kusomeshwa chini. Mtoto wa darasa la kwanza na la pili ukimwambia itifaki ya Tanzania haijui. Tumpe itifaki ya Tanzania kupita wimbo. Waliotunga nyimbo za nyingi za Tanzania na nyimbo nyingine wapo, kwa nini tusiwatumie? Mtoto tangu yupo chini, mdogo, afundishwe uzalendo wa nchi yake. Haya tunayopiga kelele humu ndani yataondoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yawe ni historia ya kuiwekea mkakati, Kama somo la historia, basi liwekewe makakati wa kuanzia chini kuja juu, liwe na uzalendo ndani yake. Haya tunayopiga nayo kelele yote yataondoka. Hivi kama mtoto wa Kitanzania, tumemjengea msingi wa uzalendo wa historia yake ya Tanzania katika somo la historia ipasavyo, unavyodhani tutapata shida na ma-engeener wa nchi hii? Unavyodhani, tutapata shida na Madaktari wa nchi hii? Wote watawajibika katika misingi ya uzalendo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uzalendo ni kila kitu. Kati ya mambo mengi tunayoyafanya, tunasahau kuwapa uzalendo. Tumwangalie Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, moja ya kitu kinachomsumbua ni uzalendo, nafsi yake imejawa na uzalendo. Uzalendo ndiyo uliokufanya kufanya mambo mazuri na yenye tija. Tuambukize uzalendo kutoka chini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutoe mifano ya dini zetu zote mbili ambazo ni kuu; dini ya Kikristo na Kiislamu, inampandikiza mtoto imani akiwa mdogo. Leo mtoto wa Kiislamu anapelekwa Chuoni toka mtoto. Dini ya Kikristo wana Sunday School, watoto wadogo wanafundishwa dini. Nini maana yake? Maana yake ni kuweka misingi ya dini akiwa mtoto. Tuweke misingi ya uzalendo kwa watoto wetu wakiwa wako chini. Hatuwezi kuweka uzalendo wakiwa juu, hawatakuwa wazalendo hata siku moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya, lakini pia aliangalie suala la riba ya mikopo kwa wanafunzi. Atumie mama fursa yake, natamani nimhamasishe kama mama, lakini kuna watu watanipa mwongozo. Kama mama atumie fursa yake, ahurumie Taifa hili, ashikane na Kiongozi wetu na Rais wetu tufanye kazi ambayo yeye anataka tuifanye. Mambo madogo tu tukiyarekebisha elimu yetu itakaa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, nashukuru kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Nichukue fursa hii ya kipekee kutoa pole kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini vile vile nitoe pole kwa familia ya mpendwa wetu Hayati Mheshimiwa Dkt. Magufuli. Pia nitoe pole kwa Watanzania wote, niwape pole Mheshimiwa Spika na Naibu Spika, niwape pole Waheshimiwa Wabunge wote. Kila mja hakika kwake atarejea, Mwenyezi Mungu ampokee Kiongozi wetu ampokelee kitabu chake kwa mkono wa kulia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mambo mengi ya kuweza kuongea kwa mpenzi wetu mpendwa wetu baba yetu Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli, kwetu Watanzania alikuwa kama taa, alikuja kwetu amefanya kazi akiwa kama taa, ameimulika Tanzania, amemulika vijana wa Tanzania, amemulika wanawake wa Tanzania, amemulika rasilimali za Tanzania, amemulika miradi ya Tanzania, amesimamia rasilimali za Tanzania akiwa yeye kama tochi, kama taa yenye mwanga mkali, kila Waziri aliyefanya kazi ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliiona taa inapomulika anajua hapa pana jambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, walisimamia kwa sababu kwetu alikuwa ni taa, lakini simuoni kama taa tu, haitoshi kwetu kuwa taa, alikuwa barabara, alikuwa njia, tumepita viongozi vijana akituonesha na kutufunza huu ndiyo uongozi, akitufunza ujasiri, akitufunza jinsi kiongozi anavyopaswa kuwa, ametufunza kuwa wakakamavu, ametufunza mambo mengi, kwangu nimeona kama ni njia, kwetu amekua njia. Nadhani wengi ni mashahidi Watanzania walipokuwa wakitembea barabarani alikuwa njia, kwetu sisi tumepita kwake kama njia.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niseme Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwetu amekuwa faraja, alikuwa faraja ya wanyonge, alikuwa jibu la wanyonge, alikuwa jibu la maskini, alikuwa jibu la akinamama wajawazito, alikuwa jibu la kumtua mwanamke ndoo kichwani. Kwetu alikuwa jibu, Mungu alimleta kwetu japo amefanya kazi kwa muda mfupi, lakini naamini dhamira yake ya kweli ametuacha sisi tumalize kazi. Tutahakikisha tunamuenzi kwa kupita kwenye njia ambazo yeye alitaka tupite, tutamuenzi kwa kuwa mwanga na sisi viongozi tuliokuwemo humu kama yeye alivyoangaza. Naamini Waheshimiwa Mawaziri wamekuwa na vitu vingi kutoka kwake wamekuwa na mitazamo mingi kutoka kwake watafuata njia ambayo yeye alitaka sisi tupite.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kwa jinsi ya kipekee nimpongeze Mama yetu, Mama Samia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, niseme Mama Samia Mheshimiwa Rais alikuwa tuko naye hapa Bungeni, sisi tukiwa kama wanawake hatuna hofu juu yake, hatuna mashaka juu yake, tuna uhakika atatuvusha na tutafika salama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka, kama kumbukumbu zangu ziko vizuri, kuna maneno ndani ya nafsi yangu kila ninapokaa yanakuja mara kwa mara, siku Mheshimiwa Mama Samia tuko kwenye kama sikosei kwenye kuapishwa, Waziri Mkuu mara hii tuko Ikulu alipata fursa ya kuzungumza, alizungumza maneno machache, lakini wakati anazungumza Mheshimiwa Rais wetu Hayati Dkt. Magufuli alikuwa yupo amekaa kitako, akatuambia baba umetufunza, tulichelewa kukufahamu, lakini kwa sasa tumekufahamu, tumekuelewa, alimwambia maneno hayo akiwa Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Magufuli Hayati alikuwa yu hai aliyazungumza mazungumzo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mazungumzo yale ndani ya nafsi yangu aliyoyazungumza Mama Samia yanaimba ndani ya nafsi yangu nikiamini kama aliweza kuyatamka akiwa yu hai, akisema tumekufahamu, tumekuelewa tutachapa kazi tuko na wewe, naamini hata sasa ndani ya nafsi yake bado maneno hayo yapo na ya hai, yanafanya kazi. Tuseme sisi kama wanawake tunamuunga mkono, kama Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tunamuunga mkono na tutafanya naye kazi. Tuwatoe hofu Watanzania uwezo na ukubwa wa kufanya kazi Mama Samia unatosha, tutafanya nae kazi kwa jitihada zetu zote. Akiwa mama amebeba uchungu wa wanawake wote anao, akiwa mama amebeba uchungu wa watoto, akiwa mama amelibeba Taifa kwa uchungu wa mama anaugua na Taifa akiwa kama mwanamke hatuna mashaka nae. Tunajua anaumia kama mwanamke, tunajua atapita kwenye misingi aliyopita Rais wetu, tunajua atatembea kwenye misingi ya Rais wetu, hatuna mashaka nae. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuseme tunachukua fursa hii tena kumpongeza tunamtakia kila heri, Mwenyezi Mungu amnyooshee, ampe kauli ambazo Taifa letu linataka, ampe majibu ya Watanzania, aendelee kusimama nae akiwa kama mwanamke, lakini kama alivyosema maneno yake yeye ni mwanamke wa jinsia kwamba yeye ni mwanamke, ila anauwezo wa kufanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo maneno machache naomba nichukue fursa hii ya kukushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. TAUHIDA C. GALLOS Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuweza kunipatia fursa hii ya kuweza kuchangia Wizara hii ya TAMISEMI. Nichukue fursa hii kwanza kabisa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Manaibu wake. Mheshimiwa Waziri dada yetu dada Ummy Mwalimu nikupongeze kwa nafasi hii uliyopewa ya Wizara hii ya TAMISEMI. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwa tunakufahamu hatuna mashaka na uwezo wako tunaamini kwenye Wizara hii utatuvusha vizuri. Hatuna mashaka kwasababu hufanyi majaribio juu ya kazi hii tunajua umekuja kufanya kazi na utachapa kazi. Ikiwa sisi kama wenzio kuna baadhi ya mambo tukwambie ili uweze kuyafanyia kazi vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri pamoja na pongezi lakini kwa sehemu lazima tukupe pole, pamoja na pongezi zote zilizo toka hapa kwa Wizara hii tukupe pole.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunaendelea kukuombea unajua kwa sehemu kubwa wanawake wenzio ndani ya Bunge tunavyokuunga mkono. Tutaendelea kukuombea Mwenyezi Mungu akujalie, akutie nguvu, akupe ujasiri, uweze kuisaidia Taifa letu. Uweze kutuvusha kama wanawake, uweze kutuvusha kama wabunge wenzio tuweze kwenda salama kwenye eneo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya TAMISEMI ni kubwa na ina mambo mengi. Mheshimiwa Waziri kwanza kabisa nianze kwa kusema wizara hii pamoja na kazi nyingi inayofanya tunaomba mpate muda wa kufanya vipindi kwenye TV hususani wa kutoa elimu kwa wananchi. Wananchi wengi hawafahamu tafsiri ya Hati Chafu na Hati Safi, wengi wao wanatafsiri tofauti na ilivyo ndani ya tafsiri ya Hati Chafu na Hati Safi. Niombe ukipata fursa kama kutakuwa na vipindi andaeni vipindi vya kuwaelewesha wananchi tafsiri za Hati Safi na Hati Chafu. Kwasababu tafsiri hii inaenda ni kitaalam zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wengi wanaposikia Halmashauri nyingine imepata Hati Chafu wakiamini kwamba kuna mambo mabaya, mabaya yaliyopitiliza lakini kuna baadhi ya Halmashauri zinapata Hati Safi iwaje ndani ya halmashauri hizo zina upigaji na miradi mibovu ambayo tunaishuhudia ndani ya macho yetu. Fursa hiyo tumeipata Wabunge kwasababu tunaenda kukagua miradi, wakati tunakwenda kukagua miradi tunakutana na Hati Safi ingawa halmashauri hiyo ina miradi mibovu na utekelezaji wa miradi ya wananchi ipo sifuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na Mheshimiwa Waziri takribani wapigaji wote wana utalaamu wa kutengeneza hati safi kwasababu wanazifahamu zinapatikana vipi. Mheshimiwa Waziri tunaomba kwenye haya yafanyanyieni uchunguzi wa kina lakini wapeni taaluma ya kutosha wananchi wapate kujua tafsiri za Hati Safi na Hati Chafu. Watu ambao wanapata Hati Chafu wanakuaje na wanaopata Hati Safi inakuaje wakapata zile Hati. Hata sisi tunavyopangiwa Kamati kuna muda zilikuwa zinatupa shida kutafsiri hizi Hati, lakini kwa kuwa tunapewa elimu na taaluma ya kutafsiri hizi Hati huwa tunaelewa kazi zinakwendaje. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la asilimia 10 ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Mheshimiwa Waziri tunakuomba shughulika na hizi asilimia 10 za wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, hili ndiyo jibu la Watanzania. Kama mikopo itatolewa ipasavyo, kama wanawake, vijana na wenye mahitaji maalum watawezeshwa ipasavyo, Tanzania tutapiga hatua, Halmashauri zitasaidia viongozi wetu kufanya kazi vizuri. Mheshimiwa Waziri ana mambo na kazi nyingi, namshauri atenge vipaumbele aone ataivusha vipi Tanzania, afanye kazi kwa kumsaidia Rais wetu. Nashauri Waziri aweke vipaumbele kwamba ndani ya mwaka mmoja au miwili vitu gani anaweza akavifanyia kazi na vikaleta jibu ndani ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, siku zote nilizokaa ndani ya Bunge hili nimekuwa mjumbe wa Kamati ya LAAC, sikuwahi kuona kuna jibu sahihi kuhusiana na asilimia 10. Pamoja na sheria tuliyoipitisha kwamba lazima kila halmashauri watenge fedha lakini bado jibu halipo. Halmashauri hazifikishi fedha kwa walengwa, fedha za mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum haziendi ipasavyo. Naomba Wizara walichukue na waliangalie kwa jicho la kipekee ili liweze kufanyiwa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna jambo tofauti, kuna baadhi ya Wakuu wa Mikoa wanashindwa kuelewa kwamba wao ni sehemu ya zile halmalshauri, wanadhani halmashauri ipo peke yake na wao wako peke yao. Kuna muda wanapoitwa utashangaa Mkuu wa Mkoa anawaambia halmashauri wajibikeni wakati ule ni uwajibikaji wa pamoja, wanajihisi wao siyo sehemu ya zile Halmashauri. Kuna baadhi ya Wakuu wa Mikoa wanafurahi wanapoziona halmashauri zinafanya vibaya na kuzitia madoa wakati wao ni sehemu ya halmashauri zile kufanya vibaya. Kama utapata muda itisha mkutano wa pamoja, Wakuu wa Mikoa, Wakurugenzi, wajue wanaisimamia Serikali ndani ya mkoa wanapaswa kwenda pamoja kwa faida ya wananchi na siyo kujinufaisha wao na kutengeneza migogoro ndani ya mikoa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nigusie suala zima la elimu, Wabunge wengi wamechangia, liangalie lilivyokuwa la pekee, kila Mbunge anayesimama kwa namna yoyote ile lazima ataigusa elimu. Kuna shule ndani ya Tanzania hii mwalimu yupo mmoja na tatizo ni dogo tu linaweza likapata ufumbuzi, kuna njia rahisi za kupata ufumbuzi. Kuna walimu unawapeleka Liwale, mwaka juzi nilichangia na hili nililizungumza, unamchukua mwalimu wa Dar es Salaam, mtoto aliyezaliwa Dar es Salaam unampeleka Liwale anashindwa kufanya kazi lakini Liwale ileile kuna walimu wanaomba nafasi zile hawapewi nafasi za kufanya kazi na wapo tayari kuisaidia Liwale, wapo tayari kusaidia eneo lao. Unamchukua mtoto wa Kahama unaenda kumpeleka Tanga akafanye kazi, uwezo wa kusema tunamtafutia nyumba hatuna, uwezo wa kusema tunamtafutia usafiri hatuna, unapomuacha kwao Shinyanga afanye kazi atakaa kwa mzee wake na kula ataisaidia Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nashauri Wizara itengeneze njia mbadala za kusaidia Serikali. Mheshimiwa Ummy Mwalimu kati ya watu niliofurahishwa na hii nafasi uliyopewa mmoja mimi, naamini utachukua maoni yetu na kuyafanyia kazi. Suala la kuwapangia walimu waende kwenye sehemu sahihi halihitaji fedha wala bajeti bali linahitaji mpango na mpango wenyewe ni rahisi. Mchukue watoto ndani ya mkoa husika wanaotaka kufanya kazi sehemu ile wapeni nafasi wafanye kazi, tuache mambo haya yanayoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la elimu, kero yangu nyingine kubwa inayonisumbua ni kuhusu vibali. Nadhani halmashauri ndizo zinazotoa vibali kwa nini mpaka leo Tanzania tunatoa vibali vya kuanzisha bar na shule iko hapo hapo? Tunatengeneza nini? Tuangalie hatuwajengi watoto wa Tanzania bali tunawabomoa. Unapotaka kutoa kibali cha bar angalia mazingira husika, unampelekeaje mtoto bar na shule ipo hapo hapo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi/Vigelegele)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. TAUHIDA C. GALLOS: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii kuweza kuchangia. Kwanza kabisa, nianze kwa kukupongeza wewe mwenyewe binafsi kwa kuteuliza na chama chako, Chama cha Mapinduzi, lakini vilevile kuweza kupata kura za kishindo kwa Wabunge. Sambamba na pongezi hizo nimpongeze Naibu wako ambaye ni msaidizi wako kwa kuchaguliwa pia naye na Wabunge kwa kura nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mchango wangu nitajielekeza kwenye matumizi ya miradi ya halmashauri. Halmashauri imekuwa na kipindi cha utekelezaji wa fedha. Kulikuwa na mambo kadhaa sugu ambayo yanaisumbua halmashauri. Kwanza, tulikwenda na tulipita kwenye awamu ya Wanasheria ambao walikuwa wakisababisha matatizo makubwa ndani ya halmashauri zetu. Tulipotoka hapo tukaja na ugonjwa wa Mfuko wa asilimia 10 ambao haukuwa na usimamizi mzuri; kwa sehemu haujapona moja kwa moja, lakini kwa sehemu kidogo kuna unafuu si asilimia 100 lakini asilimia zaidi ya 60 kidogo mabadiliko yapo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna ugonjwa ambao kwa sasa unasumbua Halmashauri zetu. Ugonjwa huo ni matumizi mabaya ya fedha; kuchukua fedha za Halmashauri kuwekeza kwenye majengo na kutokuyamaliza. Ugonjwa huu umekuwa tatizo ndani ya Halmashauri zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, fedha nyingi za wananchi zinazokusanywa kwa kodi zinaenda kutengenezwa miradi ambayo haiishi, inakaa zaidi ya miaka mitatu mpaka mitano bila ya kumalizika. Nitoe mfano kama wa Halmashauri Tatu ya toka mwaka 2012; kuna Bwalo la Chakula, Chamwino; mradi wa Babati Mjini - nyumba za Waganga; mradi wa ukumbi - Mpwapwa. Hiyo ni baadhi ya miradi ambayo ndani ya Halmashauri zetu zimetumia fedha nyingi lakini miradi haikumalizwa.
Mheshimiwa Spika, kuna aina za miradi ndani ya Halmashauri zetu; kuna miradi ya Serikali, kuna miradi ya wananchi na miradi ya watendaji. Miradi ya Watendaji mara nyingi huwa haiishi, kwa sababu huwa na miradi yenye fedha nyingi ambayo haiihitajiki na wananchi, siyo malengo ya wananchi, siyo mtazamo wa Serikali; nao huianzisha miradi ile iwe ni njia au kichochoro cha kufanikisha mambo yao. Zinachukuliwa fedha kwa mamilioni lakini bado unakuta zimeenda kutumbukizwa sehemu toka mwaka 2012 na ipo miradi mingine zaidi ya mwaka 2012 haimalizwi.
Mheshimiwa Spika, imebidi sasa tuiwekee mkazo. Mheshimiwa Rais wetu amekuwa mfano kwenye miradi. Tuchukulie mfano wa reli ambao sasa hivi unamaliziwa na Mheshimiwa Rais na bado anapeleka fedha kumaliza miradi hii. Kama ni miradi ambayo ina malengo na inahitajika kwa wananchi sielewi kuna tatizo gani la Halmashauri kila mwaka wanatenga fedha kuanzisha miradi mipya na miradi mingine kuendelea kubaki ikiwa ni miradi ambayo haifanyiwi kazi na pesa ya wananchi inapotea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, miradi mikubwa inayohitajika kwa wananchi ni hospitali, shule; hiyo ndiyo miradi wanayoihitaji wananchi. Leo unaenda kuchukua fedha unaipeleka Mpwapwa unaenda kuweka hall unategemea mtu wa Mpwawa kumkodisha hall akafanye shughuli kwa shilingi milioni tatu, itaingiza wapi fedha hizo? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, chukulia inaenda kujengwa nyumba ya Mganga vyumba vitatu, inachukua miaka minne bila kwisha, lakini fedha ya wananchi ipo pale tayari imeshakaa. Tunaishauri Serikali kuondokana na matumizi mabaya ya fedha ambapo wananchi wanazihitaji na wanahitaji zifanyiwe kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua fursa hii kuunga mkono hoja ya Kamati yetu ya LAAC. (Makofi)