Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Subira Khamis Mgalu (93 total)

MHE. ABDALLAH A. MTOLEA (K.n.y MHE. ISSA A. MANGUNGU) aliuliza:-
Je, ni lini miradi ya umeme yenye zabuni Na. PA/001/2015/DZN/W/12 maeneo ya Chamazi Dovya, Kwa Mzala 1 – 3, Mbande kwa Masista na Chamazi Vigoa itakamilika ili wananchi wa maeneo hayo wapate umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mradi tajwa hapo juu katika maeneo yaliyotaja Mheshimiwa Mbunge ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Chamazi Dovya kulikuwa na miradi mitatu na yote imekamilika. Kazi ya kupeleka umeme ilijumuisha ujenzi wa kilometa 3.297 za ujenzi ya njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 11, kilometa 1.4 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 na ufungaji wa transfoma nne za KVA 100 na transfoma mbili za ukubwa wa KVA 200 kila moja. Miradi hiyo mitatu iligharimu jumla ya shilingi 585,271,539 na ilikamilika kati ya Juni, 2016 na Januari, 2017 na kwa sasa wananchi wa maeneo hayo wanapata umeme.
Mheshimiwa Spika, Mbande kwa Masista kuna miradi mitatu; Masista Magogo Na. 1, Masista Magogo Na. 2 na Masista Magogo Na. 3 na kazi ya kupeleka umeme ilijumuisha ujenzi wa kilometa 3.5 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 11, kilometa 15.8 za njia umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 na ufungaji wa transfoma tatu zenye ukubwa wa KVA 100 na transfoma tatu za ukubwa wa KVA 200 kila moja.
Mheshimiwa Spika, miradi hiyo ka ujumla ina thamani ya shilingi 726,075,289.40. Mradi wa Masista Magogo Na. 1 ulikamilika tarehe 17 Juni, 2017 na wateja wanapata umeme. Aidha, miradi ya Masista Magogo Na. 2 na Na. 3 itakamilika mwishoni mwa mwezi Disemba, 2017.
Mheshimiwa Spika, Chamazi Vigoa kazi ya kupeleka umeme ilihusisha ujenzi wa kilometa 0.99 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 11; kilometa 3.92 za njia ya umeme wa kilovoti 0.4 na ufungaji wa transfoma tatu za ukubwa wa KVA 100 kila moja. Mradi huu wenye thamani ya shilingi 178,584,000 ulikamilika tarehe 9 Juni 2016 na wateja wanapata umeme.
MHE. MARY D. MURO aliuliza:-
Tangu mwaka 2014 TANESCO iliweka alama ya X kwenye maeneo ya Kiluvya, Kibaha hadi Chalinze kupisha ujenzi wa kupitisha umeme wa Gridi ya Taifa lakini hadi sasa hakuna fidia iliyolipwa kwa wananchi hao na pia wanashindwa kufanya uendelezaji wa maeneo hayo. Je, ni lini wananchi hao watalipwa fidia stahiki?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO inatekeleza mradi mkubwa wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 400 kutoka Kinyerezi Dar es Salaam kupitia Chalinze, Segera hadi Arusha yenye urefu wa kilometa 600. Pia mradi huo utahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wenye msongo wa kilovoti 220 kutoka Kibaha hadi Bagamoyo yenye urefu wa kilometa 40 na kutoka Segera hadi Tanga yenye urefu wa kilometa 60. Mradi huu pia unahusisha ujenzi wa vituo vya kupoozea umeme vya Chalinze, Segera, Kange na Zinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo ya mradi huu ni kuongeza upatikanaji wa umeme katika Ukanda wa Mashariki na Kaskazini mwa nchi kutoka kwenye mitambo ya kuzalisha umeme ya Kinyerezi. Gharama za mradi huo ni dola za Marekani milioni 693 ambazo zitagharamiwa kwa mkopo kutoka benki ya Exim-China kwa asilimia 85 na Serikali ya Tanzania asilimia 15.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kutathmini mali za wananchi watakaopisha mradi huo kutoka Kibaha hadi Chalinze imekamilika na kuidhinishwa na Mtathmini Mkuu wa Serikali. Jumla ya shilingi bilioni 21.6 zitahitajika kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi wapatao 855 wa Halmashauri za Kisarawe, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini, Bagamoyo ikiwemo eneo la Kiluvya. Fidia hiyo italipwa na Serikali na fedha hizo zimetengwa katika bajeti ya Wizara kwa mwaka 2017/2018. Taratibu zote za uandaaji taarifa na majedwali ya malipo ya fidia zimekamilika na malipo yamepangwa kulipwa katika mwaka huu wa fedha 2017/2018.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA (K.n.y. MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE) aliuliza:-
Maeneo ya Munguatosha na Hondogo ni baadhi ya maeneo ambayo yanahitaji transfoma ili umeme uwake.
Je, Serikali ina mpango gani juu ya kupeleka transfoma katika maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Hondogo kimewekwa katika mradi wa REA Awamu ya III kupitia Mradi wa Densification Awamu ya Kwanza ulioanza mwezi Machi, 2017 unaotekelezwa na kampuni ya STEG. Mkandarasi tayari amesimamisha nguzo 111 na kuvuta waya wenye urefu wa kilometa 4.5. Hatua inayofuata ni ufungaji wa transfoma yenye uwezo wa kVA 50 itakayofanyika mwishoni mwaka mwezi Novemba, 2017. Wateja wapatao 65 wanatarajiwa kuunganishiwa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kitongoji cha Munguatosha kilichopo katika Kijiji cha Makore kimejumuishwa na kitapatiwa umeme kupitia REA awamu ya III chini ya Grid extension utakaotekelezwa na kampuni ya Sengerema Engineering Group Limited.
Kazi ya kupeleka umeme katika Kitongoji cha Munguatosa inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa mbili, ufungaji wa transfoma yenye uwezo wa kVA 50 pamoja na kuunganisha wateja wapatao 46. Utekelezaji wa mradi huu ulianza mwezi Julai, 2017 na utakamilika mwezi Juni, 2019.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA aliuliza:-
Katika Mkoa wa Mtwara kuna tatizo kubwa la kukatika kwa umeme mara kwa mara jambo ambalo linaathiri wananchi ikiwemo wafanyabiashara ambao wanategemea sana umeme na hivyo kusababisha wakati mwingine biashara hizo kuharibika na kuwasababishia hasara wananchi hao.
Je, ni lini Serikali itawahakikishia wananchi wa Mtwara kupata umeme wa uhakika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shamsia Aziz Mtamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini wanapata umeme wa uhakika ili kuboresha maisha yao. Serikali kupitia TANESCO imeweka jitihada kubwa kuhakikisha kuwa umeme wa kutosha katika Mikoa ya Mtwara na Lindi unapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kufanya ukarabati mkubwa wa mitambo yote tisa iliyopo Mtwara yenye uwezo wa kuzalisha megawati 18. Ukarabati huu ulianza mwishoni mwa mwezo Oktoba, 2017 na utakamilika mapema mwezi Desemba, 2017. Gharama ya matengenezo kwa mitambo yote ni shilingi 4,800,000,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ukarabati huo, Serikali imeagiza mitambo miwili mipya kutoka Kampuni ya Caterpillar yenye uwezo wa kuzalisha jumla ya megawati nne kwa gharama ya shilingi 8,300,000,000. Ufungaji wa mitambo hiyo unatarajiwa kuanza mwezi Januari, 2018 na kukamilika mwezi Aprili, 2018. Mitambo hiyo itaongeza uwezo wa mashine zilizopo kufikia megawati 21.75.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO imeanza utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa megawati 300 kwa kutumia gesi asilia Mkoani Mtwara. Kazi inayoendelea kwa sasa ni kukamilisha upembuzi yakinifu kupitia Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Japani (JICA). Mradi huo unategemewa kuanza mwezi Aprili, 2018 na kukamilika mwezi Desemba, 2019. Mradi huu utakapokamilika utatoa suluhisho la kudumu la upatikanaji wa umeme wa kutosha katika Mikoa ya kusini ikiwa ni pamoja na Lindi na Mtwara.
MHE. EDWARD F. MWALONGO (K.n.y. MHE. GODFREY MGIMWA) aliuliza:-
Tatizo la umeme bado ni kubwa licha ya jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali.
Je, ni lini Serikali itatatua tatizo hili na hatimaye kuvipatia umeme Vijiji vya Kipera, Lupalama, Itagutwa na Lyamgungwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatarajia kuvipatia umeme Vijiji vya Kipela, Lupalama, Itagutwa, Ikongwe na Lyamgungwe katika Awamu ya Tatu ya uetekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini (REA III) inayoendelea kwa sasa. Aidha, kwa Mkoa wa Iringa miradi hiyo inatekelezwa na mkandarasi Kampuni ya Sengerema Engineering Group na tayari yupo katika eneo (site) akifanya upimaji wa awali kwenye vijiji tajwa pamoja na vijiji vingine 145 vya Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivyo tajwa inajumuisha ujenzi wa njia za umeme wa msongo wa kilovolti 33 na 11 zenye urefu wa kilometa 22; msongo wa kilovolti 0.4 yenye urefu wa kilometa 18; na uwekaji wa transfoma tisa pamoja na kuwaunganisha umeme wateja 215. Gharama ya kutekeleza miradi hiyo ni jumla ya shilingi bilioni 2.3.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA aliuliza:-
Kasi ya usambazaji umeme vijijini ni kubwa, lakini katika baadhi ya maeneo, miundombinu inayotumika hasa nguzo hairidhishi.
Je, Serikali inaweza kutuambia ni viwango gani (standards) vinavyotumika katika utafutaji wa nguzo hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa miradi ya usambazaji umeme vijijini, Serikali imekuwa ikihimiza na kuzingatia ubora wa vifaa vinavyotumika hasa nguzo. Nguzo zinazotumika kwenye miradi hiyo hununuliwa kutoka viwanda mbalimbali vya hapa nchini na awali baadhi zilikuwa zinatoka nje ya nchi.
Wakati wa ununuzi Shirika la Umeme nchini TANESCO hutoa viwango vya ubora wa nguzo kwa viwanda vinavyohitajika na vinavyozingatia viwango vya kimataifa. Kwa kuzingatia viwango hivyo, nguzo kwa ajili ya usambazaji na usafirishaji wa umeme zinatakiwa kuwa na urefu kati ya mita tisa hadi 18 na kipenyo kati ya milimita 130 hadi 308.
Mheshimiwa Naibu Spika, wazalishaji hutumia dawa bora kuzalisha nguzo hizo na TANESCO hufanya ukaguzi kabla ya kuanza kutumika ili kujiridhisha katika ubora wake.
MHE. DAVID E. SILINDE aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itakamilisha miradi ya umeme katika vijiji ambavyo havijafikiwa katika Halmashauri ya Momba?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ni kufikisha umeme katika vijiji vyote visivyo na umeme nchini ikiwemo vijiji vya Wilaya ya Momba ifikapo Juni, 2021. Katika Wilaya ya Momba jumla ya vijiji 27 vitapatiwa umeme kupitia mzunguko wa kwanza wa awamu ya tatu ya miradi ya kusambaza umeme vijijini. Vijiji hivyo ni pamoja na Ikana, Nakawale, Ipanga, Mpui, Mfuto, Machindo, Muungano, Samang’ombe, Tundumakati, Unyamwanga, Nello, Tukuyu, Mlimani, Majengo Mapya, Ihanda na Migombani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za mradi zinazotekelezwa na Kampuni ya STEG International ambazo zinahusisha ujenzi wa kilometa 60 za umeme msongo wa kilovoti 33 na kilometa 108 za njia za umeme msongo kilovoti, kufunga transfoma 54 na kuunganisha wateja 1,773. Gharama ya mradi inakadiriwa kuwa shilingi 6,607,000,000 na mradi unatarajiwa kukamilika mwezi Aprili, 2019.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vitakavyobakia katika mzunguko wa kwanza wa REA III vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa REA-III iunaotarajiwa kuanza mwezi Aprili, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. PROF. JUMANNE A. MAGHEMBE aliuliza:-
Miradi ya REA I na II katika Wilaya ya Mwanga haikukamilika na fedha zilizokuwa zimepangwa hazikutumika:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia umeme wananchi waliopitiwa na umeme huo bila kufungiwa?
(b) Je, Awamu ya III ya REA iliyozinduliwa Mwanga, mwezi Septemba, 2017 itaanza kutekelezwa lini?
elezaji wa REA Awamu ya I na II Wilaya ya Mwanga
MHE. PROF. JUMANNE A. MAGHEMBE aliuliza:-
Miradi ya REA I na II katika Wilaya ya Mwanga haikukamilika na fedha zilizokuwa zimepangwa hazikutumika:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia umeme wananchi waliopitiwa na umeme huo bila kufungiwa?
(b) Je, Awamu ya III ya REA iliyozinduliwa Mwanga, mwezi Septemba, 2017 itaanza kutekelezwa lini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Jumanne Abdallah Maghembe, Mbunge wa Mwanga, lenye Sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya vijiji 38 kati ya vijiji 44 vya Wilaya ya Mwanga vilipata umeme kupitia Awamu ya II ya Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini ambapo wateja zaidi ya 2,241 waliunganishiwa umeme. Aidha, vijiji sita vilivyosalia havikuweza kupatiwa umeme kutokana na Mkandarasi, Kampuni ya SPENCON, aliyekuwa anafanya kazi hiyo kushindwa kukamilisha kazi hiyo na mkataba wake kusitishwa mwezi Disemba, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imempata Mkandarasi Kampuni ya M/S Octopus Engineering Limited atakayeikamilisha kazi ya kupeleka umeme katika vijiji vilivyosalia kwa awamu ya pili. Kazi hizo zimeanza rasmi mwezi Januari, 2018 na zitakamilika ndani ya miezi sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya Tatu katika Wilaya ya Mwanga ulianza mwezi Oktoba, 2017 chini ya Mkandarasi Kampuni ya Urban and Rural Engineering Services Limited. Kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 10.98; njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 urefu wa kilometa 24; ufungaji wa transformer 12 za kVA 50; pamoja na kuunganisha wateja wa awali 347. Gharama za mradi ni Dola za Marekani milioni 1.7 na shilingi bilioni 12.3; mradi huu utakamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. ALLAN J. KIULA aliuliza:-
Wilaya ya Mkalama ina shida kubwa ya Nishati ya Umeme licha ya mpango wa REA II na REA III kuwepo nchi nzima:-
(a) Je, ni lini miradi iliyokuwa chini ya REA II itakamilika baada ya kutekelezwa katika Kata ya Ibega, Mwangeza na Mpambala?
(b) Je, ni lini REA III itaanza Mkalama hasa ikizingatiwa mikoa yote imepata wakandarasi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Allan Joseph Kiula, Mbunge wa Iramba Mashariki, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miradi ya REA II haikukamilika katika Mkoa wa Singida ikiwemo Wilaya ya Mkalama baada ya Mkandarasi aliyekuwa akitekeleza miradi hiyo kampuni ya Spencon Services kushindwa kukamilisha kazi hiyo kama ilivyopangwa. Utekelezaji wa miradi hiyo ulifikia asilimia 65.
Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya Kampuni hiyo kushindwa kukamilisha kazi kwa asilimia 35 iliyobaki, vifaa kwa ajili ya kazi hizo vimehifadhiwa katika Ofisi ya TANESCO Mkoani Singida. Vifaa hivyo vimekabidhiwa kwa Mkandarasi aliyepewa kazi hiyo Mwezi Januari, 2018. Kazi za miradi zilizobaki zinatarajiwa kukamilika ifikapo Mwezi Agosti, 2018
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkandarasi anayetekeleza miradi ya REA III Awamu ya kwanza katika Mkoa wa Singida ni Kampuni ya CCCE-ETERN-HEI Consortium ambapo mkataba wa kazi hiyo umesainiwa Mwezi Oktoba, 2017. Kazi za miradi zilianza Mwezi Oktoba, 2017 ambapo Mkandarasi amekamilisha kazi za upimaji na usanifu wa njia za kusambaza umeme pamoja na ununuzi wa vifaa. Mzunguko wa kwanza wa mradi huu Mkoani Singida unatarajwa kukamilika ifikapo Mwezi Juni, 2019, gharama ya mradi ni shilingi bilioni 41.5 wateja zaidi ya 2,997 wanatarajiwa kuunganishiwa umeme kupitia mradi huu.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza:-
Ni muda mrefu tangu transfomer katika Kijiji cha Itengelo, Kata ya Saja imefungwa lakini umeme haujawashwa. Je, ni lini Serikali itawasha umeme katika kijiji hicho?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji cha Itengelo ni miongoni mwa vijiji vilivyonufaika na mradi wa REA Awamu ya Pili uliotelekezwa na Mkandarasi Kampuni ya M/S Sengerema Engineering Group Limited ambaye alipewa kazi ya mradi kwa Mkoa wa Njombe. Kazi zilizofanyika ni pamoja na ujenzi wa kilometa 8.5 za njia za umeme msongo wa kilovoti 33 na kilometa sita za njia za umeme msongo kilovoti kwa gharama ya shilingi milioni 564. Maradi ulikamilika mwezi Desemba, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji cha Itengelo kiliwashiwa umeme tarehe 22/08/2017 kwa kufungiwa transfomer mbili pamoja na kuwaunganisha umeme wateja 56 waliolipia.
MHE. OMARY T. MGUMBA aliuliza:-
Kata sita za Tegetelo, Kibuko, Tomondo, Tununguo, Seregete, Matuli na Mkulazi katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki hazijafikiwa na miundombinu ya umeme mpaka sasa. Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omary Tebweta Mgumba, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ni kufikisha umeme katika vijiji vyote visivyo na umeme nchini ikiwemo vijiji vya Wilaya ya Morogoro ifikapo mwezi Juni, 2019. Kupitia mzunguko wa kwanza wa awamu ya tatu ya miradi ya kusambaza umeme vijijini katika Wilaya ya Morogoro vijiji 14 vitapatiwa umeme ifikapo mwezi Aprili, 2019. Vijiji hivyo ni pamoja na Tununguo, Kibwege, Lung’ala, Kidugalo, Kinonko, Vihengele, Konde, Vigolegole, Singisa, Rudewa, Bonye, Mtego wa Simba, Muungano na Mangala.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za kupeleka umeme katika vijiji hivyo, zinajumuisha ujenzi wa kilometa 16.5 za njia za umeme msongo wa kilovolti 33 na kilometa 16 za njia za umeme msongo kilovolti 0.4, kufunga transfomer nane na kuunganisha wateja 258. Gharama ya mradi inakadiriwa kuwa shilingi bilioni 1.3. Kazi hii itatekelezwa na Mkandarasi Kampuni ya State Grid Electrical and Technical Works.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vitakavyobaki katika mzunguko wa kwanza wa REA Awamu ya Tatu vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa REA Awamu ya Tatu ambapo mradi unategemewa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE aliuliza:-
Maeneo mengi ya Halmashauri ya Chalinze yamefaidika na Mradi wa REA Awamu ya Pili lakini katika utekelezaji wa mradi huo Miji ya Kiwangwa, Hondogo, Mkange na Kibindu bado haijafikiwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuifikia miji hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Kiwangwa katika Jimbo la Chalinze umepatiwa umeme kupitia mradi uliotekelezwa na TANESCO kwa ufadhili wa Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) awamu ya kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu ulishakamilika na wateja zaidi ya 600 wameunganishiwa umeme. Kijiji cha Hondogo kimepatiwa umeme kupitia mradi wa densification awamu ya kwanza uliokuwa unatekelezwa na Mkandarasi Kampuni ya STEG international Services kutoka Tunisia. Kazi za mradi huu zimegharimu shilingi bilioni 1.16 ambapo wateja zaidi ya 66 wameunganishiwa umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji cha Mkange kitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Peri Urban utakaotekelezwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2018/2019. Mradi huu unahusisha ujenzi wa njia za umeme wa msongo wa kilovolt 33 wenye urefu wa kilometa 26 kutoka Miono hadi Saadani utakaonufaisha Vijiji vya Manda, Mazingara na Gongo. Gharama za kuvipatia umeme vijiji hivi ni shilingi bilioni tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji cha Kibindu kitapatiwa umeme kupitia njia ya umeme ya msongo wakilovolt 33 yenye urefu wa kilometa 66 kutoka shule ya sekondari Changarikwa. Njia hii ya umeme itanufaisha pia vijiji vya Kwaruhombo, Kwamduma, Kwamsanja na Kwankonje. Gharama ya kufikisha umeme katika vijiji hivi ni shilingi bilioni tano. Kazi hizi zitatekelezwa kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu, mzunguko wa pili unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwaka 2021. Ahsante. (Makofi)
MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y. MHE. JAMAL KASSIM ALI) aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kulifanyia Shirika la Umeme (TANESCO) lijiendeshe kwa faida?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jamal Kassim Ali, Mbunge wa Magomeni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) linakabiliwa na gharama kubwa za uendeshaji ambapo zaidi ya asilimia 80 ya gharama zinatokana na uzalishaji wa umeme, ukarabati wa mitambo na miundombinu mingine muhimu ya umeme. Mapato ya Shirika yamekuwa hayakidhi vya kutosha gharama za uendeshaji hususan katika maeneo ya uzalishaji wa umeme kwa kutumia mafuta mazito ambayo ni ghali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika pia linakabiliwa na tatizo la malimbizo ya madeni ya wateja wakubwa, wa kawaida na wadogo kushindwa kulipa ankara za umeme kwa wakati zikiwemo Taasisi na Mashirika ya Umma pamoja na wateja wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mikakati madhubuti ya kuliwezesha Shirika la TANESCO kujiendesha kibiashara na kuondokana na hasara. Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kuongeza uzalishaji wa umeme kwa kufanya uwekezaji katika mitambo ya kufua umeme kwa kutumia gesi asilia na maji ili kuepukana na mitambo inayotumia mafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari mipango inaendelea kuanza utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa megawati 2100 wa Rufiji Stigler’s Gorge utakaozalisha umeme kwa gharama nafuu na hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za kuzalisha umeme na kulifanya Shirika lijiendeshe kibiashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingine ni megawati 300 zitokanazo na gesi asilia eneo la Mtwara pamoja na megawati 330 katika eneo la Somangafungu Mkoani Lindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha karibuni, maeneo ya Kibiti, Ikwiriri na Ngara yameunganishwa katika gridi ya Taifa, hivyo kupelekea kupunguza gharama za uendeshaji iliyokuwa ikitokana na matumizi ya mafuta mazito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango mingine ya Serikali ni kuunganisha baadhi ya maeneo katika Gridi ya Taifa kwa utekelezaji wa miradi ya njia kusafirisha umeme kwa Mikoa ya Ruvuma, Rukwa na Kigoma na hivyo kuachana na mitambo inayozalisha umeme kwa mafuta ambayo ni ghali. Ahsante sana.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:-
Vijiji vya Nyakaboja, Kabita, Chumve, Kalemela, Kalago, Badugu na Nyaluhande vimepitiwa na nguzo na nyaya za umeme, lakini wananchi hao hawana huduma ya umeme:-
Je, ni lini Serikali itawapatia umeme wananchi wa maeneo hayo ili wasiendelee kuwa walinzi wa nguzo za TANESCO?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Raphael Masunga Chegeni, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Busega ina Vijiji 59, kati ya vijiji hivyo vijiji 18 vimepatiwa umeme kupitia miradi ya Electricity V na REA Awamu ya II. Kijiji cha Kalemela kilipatiwa umeme kupitia REA Awamu ya Kwanza. Kijiji cha Badugu kimepatiwa umeme kupitia mradi wa Electricity V na baadhi ya maeneo ya Kijiji cha Nyaluhande vimepitiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Pili.
Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Kabita, Nyakaboja na Kalago vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza ambao utekelezaji wake umekwishaanza kupitia Mkandarasi White City Guangdong JV Limited. Kazi za mradi wa kupeleka umeme katika Wilaya ya Busega zinajumuisha ujenzi wa kilometa 49.7 za njia ya umeme, msongo wa kilovoti 33, kilometa 116 za njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transforma 58 na kuunganisha wateja wa awali 1,783. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 5.5. Mradi unatarajiwa kukamilika Julai, 2019.
Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Chumve pamoja na vijiji vingine vilivyobaki vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa pili unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021. Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA (K.n.y. MHE. PHILIPO A. MULUGO) aliuliza:-
Wilaya ya Songwe ina jumla ya vijiji 43 lakini mpaka sasa hakuna kijiji hata kimoja chenye umeme kwa mpango wa umeme wa REA toka awamu ya kwanza na ya pili:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha inatoa upendeleo maalum kwa vijiji vya wilaya hii mpya katika awamu ya tatu ya REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Philipo Augustino Mulugo, Mbunge wa Songwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Jimbo la Songwe lina jumla ya vijiji 43 ambapo kati ya vijiji hivyo, sita vilipatiwa umeme kupitia mradi wa REA awamu ya kwanza na Vijiji 14 vya Ilasilo, Galula, Kanga, Mbala, Iseche, Majengo, Tete, Ifenkenya, Nahalyongo, Chang’ombe, Ifuko, Maamba, Songambele, Totowe na Mbuyuni vilipatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Pili.
Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Itiziro, Undinde, Mbangala, CHUDECO, Kambarage, Ilasilo, Kaloleni, Ndanga na Mwagala ni miongoni mwa vijiji 14 vinavyotarajiwa kunufaika na utekelezaji wa mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa kwanza. Utekelezaji wa mradi huu ulianza mwezi Julai, 2017 ambapo Mkandarasi M/S STEG International Services alipewa kazi za mradi katika Mkoa wa Songwe. Kazi zinazofanyika kwa sasa ni pamoja na kuleta vifaa katika maeneo ya mradi. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2019.
Mheshimiwa Spika, wigo wa mradi katika Jimbo la Songwe unajumuisha ujenzi wa kilometa 46.64 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 na kilometa 52.09 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transforma 14 na kuunganisha wateja wa awali 3,980. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 13.05.
Mheshimiwa Spika, vijiji vilivyobaki vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa pili unaotarajiwa kuanza kutekelezwa mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021. Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. OMARY T. MGUMBA aliuliza:-
REA I na II ilikuwa ni kupeleka miundombinu ya umeme vijijini na baadhi ya Makao Makuu ya vijiji tu na kuacha vitongoji vya vijiji husika.
Je, Serikali ina mikakati gani ya kuwapatia umeme vitongoji vyote na vijiji vilivyorukwa katika REA I na II?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omary Tebweta Mgumba, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi wa kupeleka umeme katika vijiji vyote ifikapo mwezi Juni, 2021. Katika kufikia azma hii, Serikali inatekeleza mradi wa REA awamu ya tatu kupitia maeneo yafuatayo: kwanza, grid extension unaohusu kupeleka umeme katika vijiji vyote ambavyo havikufikiwa na miundombinu ya umeme. Mradi huu wa REA III mzunguko wa kwanza umekwishaanza. Mzunguko wa kwanza unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2019 na mzunguko wa pili unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilka mwezi Juni, 2021.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aina ya pili ya mradi wa REA ni mradi wa densification. Mradi huu umepangwa kutekelezwa katika vijiji ambavyo tayari vimefikiwa na miundombinu ya umeme lakini baadhi ya taasisi za huduma za kijamii na Vitongoji havikupata umeme wakati wa utekelezaji wa REA I na II.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aina ya tatu ni mradi wa kupeleka umeme katika vijiji nje na miundombinu ya umeme wa gridi kwa kutumia nishati jadidifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji na vitongoji vilivyorukwa wakati wa utekelezaji wa miradi ya REA I na II vitapatiwa umeme kupitia miradi ya densification na utekelezaji wa awamu ya kwanza ya miradi ya densification ulikwishaanza katika mikoa nane ya Mbeya, Songwe, Njombe, Iringa, Pwani, Tanga, Arusha na Mara. Serikali inafanya maandalizi ya densification awamu ya pili unaotarajiwa kuanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2018/2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki jumla ya vitongoji 55 vimeainishwa kwa ajili ya kupatiwa umeme kupitia densification awamu inayofuata. Mkakati wa Serikali ni kuvipatia umeme vitongoji vyote ifikapo mwezi Juni, 2021.
MHE. MARY P. CHATANDA (K.n.y. MHE. HAMOUD A. JUMAA) aliuliza:-
Serikali iliahidi kuwapa fidia wananchi waliopisha njia ya mradi wa umeme wa gesi toka Kinyerezi kwenda Arusha, Awamu ya Kwanza hadi Chalinze lakini hadi sasa wananchi hao hawajalipwa fedha zao.
Je, ni lini wananchi wa Kibaha watalipwa fidia kutoka katika fedha zilizotolewa na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano shilingi bilioni mbili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hamoud Abuu Jumaa, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) inatekeleza mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 400 kutoka Kinyerezi hadi Arusha. Mradi huu unahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 400 yenye urefu wa kilometa 664 pamoja na kilometa 40 kutoka Kibaha hadi Zinga na kilometa 60 kutoka Segera hadi Kange, Tanga. Mradi huu unahusisha ujenzi wa Vituo vya Kupoza Umeme vya Chalinze, Segera, Kange na Zinga, Bagamoyo. Mradi huu utajengwa kwa mkopo kutoka Benki ya Exim ya China.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015 kazi ya utathmini wa mali za wananchi wa Kibaha na Chalinze ilifanyika ili waweze kulipwa fidia na kupisha ujenzi wa mradi. Kazi inayofanyika kwa sasa ni kukamilisha taratibu za malipo kwa wananchi waliohakikiwa. Zaidi ya shilingi bilioni 21.56 zimetengwa katika bajeti ya mwaka 2017/2018 kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi wanaopitiwa na mradi katika maeneo ya Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini na maeneo mengine yanayopitiwa na mradi kutoka Kinyerezi hadi Chalinze. Fidia kwa wananchi hao italipwa mara tu baada ya taratibu za malipo hayo kukamilika.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA aliuliza:-
Mradi wa kupeleka Umeme Vijijini (REA) ni mradi ambao unaendelea kwa kasi kubwa nchi nzima.
Je, Serikali inaweza kutuambia ni kwa kiasi gani umeme huu umesambazwa nchi nzima (coverage) tangu mradi huu ulipoanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini imekamilisha utekelezaji wa Mradi wa REA I ambapo utekelezaji wake ulijumuisha ujenzi wa miundombinu ya umeme wa msongo wa kilovoti 11/33 wenye urefu wa kilometa 1,700; umeme wa msongo wa kilovoti 0.4/0.23 wenye urefu wa kilometa 800 na ufungaji wa transfoma 386. Jumla ya vijiji 231 vilipatiwa umeme na jumla ya wateja 22,100 waliungan`ishiwa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa Mradi wa REA II ulijumuisha ujenzi wa miundombinu ya umeme wa msongo wa kilovoti 11/33 wenye urefu wa kilometa 17,740; ujenzi wa umeme wa msongo wa kilovoti 0.4/0.23 wenye urefu wa kilometa 10,970; ufungaji wa transfoma 4,100 za ukubwa tofauti na kuvipatia umeme vijiji 2,500 na kuunganishia umeme kwa jumla ya wateja 178,641 ambao ni sawa na asilimia 71.46 ya matarajio ya wateja 250,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa azma ya Serikali ni kupeleka umeme katika vijiji vyote kufika mwaka 2020/2021, Serikali kupitia Wakala wa Umeme Vijijini (REA) mwezi Julai 2017 ilianza kutekeleza mradi wa REA III kupitia grid extension na Densification itayopeleka umeme maeneo ambayo yaliyorukwa katika utekelezaji wa REA I na II.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuunganisha umeme maeneo ya pembezoni mwa miji (Peri-urban, electrification program), kusambaza umeme katika vijiji vyote ikiwa ni pamoja vilivyo pembezoni mwa mkuza wa njia ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga na utekelezaji wa miradi ya nishati jadidifu. Utekelezaji wa miradi ya REA III kwa mzunguko wa kwanza unajumuisha ufunguji wa miundombinu ya umeme ya msongo wa kilovoti 11/ 33 yenye urefu wa kilometa 16,420; njia za umeme wa msongo wa kilo vote 0.4 lenye urefu wa kilometa 15,600; ufungaji wa transforma 6,700 na kuvipatia umeme vijiji zaidi 3,559 na kuwaunganisha wateja 300,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi mwezi Machi utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme vijijini nchini umechangia kufikia matumizi jumla ya umeme nchini (overall access) kufikia asilimia 67.5 kwa vijijini ambapo vijijini ni asilimia 49.5 kutoka asilimia mbili iliyokuwepo wakati wakala unaanza kutekeleza majukumu yake mwaka 2007 na mijini ni asilimia 97.3.
MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. KEMIREMBE J. LWOTA) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itahakikisha umeme wa uhakika kwenye Kata za Wilaya ya Nyamagana, Mkoa wa Mwanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishari napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kimirembe Julius Lwota, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Nyamagana ina jumla ya Kata 18 ambazo ni Nyegezi, Mkolani, Buhongwa, Rwanhima, Mkuyuni, Mabatini, Luchelele, Igogo, Pamba, Nyamagana, Mirongo, Isamilo, Mbungani, Mahina, Igoma, Butimba, Muhandu na Kishiri. Kata zote hizi zinapata umeme wa Gridi ya Taifa japo baadhi ya maeneo ya Kata hayana umeme wa uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO inaendelea kujenga miundombinu ya umeme na kusambaza umeme katika maeneo yote ya nchi yetu. Katika bajeti ya mwaka 2017/2018 Shirika la Umeme (TANESCO) limetenga jumla ya shilingi bilioni nane na milioni mia saba thelathini kwa ajili ya kujenga, kukarabati na kuboresha miundombinu ya umeme ya Mkoa wa Mwanza ikiwepo Wilaya ya Nyamagana na Kata zake ili kuhakikisha umeme unapatikana kwa uhakika. Hadi kufikia mwezi Machi, 2018 jumla ya nguzo 519 za umeme wa kati wenye msongo wa kilovoti 11 na 33 na nguzo 188 za msongo wa voti 400 katika Kata za Nyamagana na maeneo mengine ya jiji la Mwanza vimebadilishwa, pia vikombe 807 vilikuwa vimevunjika vimebadilishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha kilometa 33 za msongo wa kati na madogo zimesafishwa kwa kukata miti pamoja na kubalisha waya kwa kilometa 22 zilizokuwa zimechakaa. Zoezi hili la ukarabati linaendelea ili kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maboresho hayo yamewezesha kuimarika kwa upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Mwanza ukilinganisha na kipindi cha nyuma. Aidha, kukamilka kwa mradi mkubwa wa kusafirisha umeme wa msongo kilovoti 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga kumechangia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa umeme katika Mkoa wa Mwanza. Zoezi la ukarabati na matengenezo ya miundombinu ya umeme ni endelevu na kiasi cha fedha shilingi bilioni nne kimependekeza katika bajeti ya mwaka huu 2018/2019 kwa ajili kuboresha miundombinu ya umeme ya uhakika Jijini Mwanza.
MHE. ZAINABU M. AMIRI aliuliza:-
Je ni lini Serikali itapunguza bei ya gesi kwa matumizi ya majumbani ili kuwawezesha wananchi wengi zaidi kutumia gesi kwa matumizi yao ya nyumbani na kuondokana na matumizi ya kuni na mkaa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Mndolwa Amiri, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, gesi iliyogunduliwa nchini ni gesi asilia (natural gas) ambayo husafirishwa kutoka kwenye visima vya gesi hadi kwa watumiaji kupitia mabomba. Mpaka sasa watumiaji wakubwa wa gesi hapa nchini ni viwanda na mitambo ya kufua umeme. Mradi wa majaribio wa gesi asilia kwa ajili ya matumizi ya nyumbani ulianza kupitia mradi wa mfano (pilot project) ambapo nyumba 70 zilizopo Mikocheni Jijini Dar es Salaam zimeunganishwa na gesi kwa matumizi ya nyumbani.
Mheshimiwa Spika, hivi sasa gesi inayotumiwa na wananchi kupikia majumbani ni Liquefied Petroleum Gas (LPG) ambayo huagizwa na wafanyabiashara kutoka nje kama ilivyo katika mafuta ya petrol, diesel na mafuta ya taa au ndege. Gesi hii hujazwa katika mitungi kwa ujazo tofauti tofauti na gharama ya gesi hii inategemeana na soko la dunia.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhamasisha wawekezaji katika sekta ya gesi kwa ajili ya matumizi ya majumbani ili kuleta ushindani katika sekta hii. Mpaka sasa makampuni mengi yameanza kujenga miundombinu ya gesi katika sehemu mbalimbali za nchi na kuonesha nia ya kushirikiana na Serikali katika kusambaza gesi asilia nchini.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TPDC imeanza matayarisho ya kutekeleza mradi wa kuunganisha gesi majumbani ambapo awamu ya kwanza ya mradi huo utapita katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam na Mtwara na baadaye katika mikoa mingine ya nchi yetu. Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza:-
Je, ni lini Vijiji vya Jeje, Kashangu, Idodyandole, Mbugani, Aghondi, Mabondeni, Kitopeni, Ipande, Muhanga, Damwelu, Kitaraba, Kazikazi, Kintanula na Rungwa vitapatiwa umeme katika Mradi wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme katika vijiji vyote vya Tanzania Bara ambavyo havijafikiwa na miundombinu ya umeme ili vifikiwe na umeme ifikapo mwezi Juni, 2021.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Manyoni Magharibi lina vijiji vipatavyo 39 ambapo vijiji 11 vimefikishiwa miundombinu ya umeme. Vijiji 10 vya Kamenyanga, Kayui, Jeje, Songa Mbele, Njirii, Kashangu, Idodyandole, Sanjaranda, Ziginali na Ipanga vimewekwa katika mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza. Utekelezaji wa mradi huu umekwishaanza na mkandarasi anayefanya kazi hii katika Mkoa wa Singida aitwaye CCCE-ETERN Consortium anatarajia kukamilisha kazi Juni, 2019. Kazi za ujenzi zinajumuisha ujenzi wa kilometa 22.4 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 na kilometa 36 za njia za umeme wa msongo kilovoti 0.4/0.23, ufungaji wa transfoma 18 na uunganishwaji wa wateja 662. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji 18 vilivyobaki vikiwemo vya Mbugani, Aghondi, Maondeni, Kitopeni, Ipande, Muhanga, Damwelu, Kitaraba, Kazikazi, Kitamula na Rungwa vitaanza kupelekewa umeme kupitia mradi huu mzunguko wa pili kuanzia Julai, 2019 na kukamilika Juni, 2021.
MHE. ISSA A. MANGUNGU aliuliza:-
(i) Je, ni lini ujenzi wa kituo kidogo cha kupoza umeme (substation) ya Mbagala utakamilika?
(ii) Je, makubaliano ya mkataba wa ujenzi wa kituo hicho ulikuwa wa muda gani?
(iii) Je, mkandarasi wa mradi huo yupo ndani ya muda au amechelewesha kazi kwa mujibu wa mkataba na je ni hatua gani zimechukuliwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
• Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika Jiji la Dar es Salaam hasa maeneo ya Mbagala, Shirika la Umeme nchini (TANESCO) mwezi Februari, 2018 kupitia Mradi wa TEDAP (Tanzania Energy Development and Access Expansion Project) lilikamilisha utekelezaji wa mradi wa uboreshaji wa njia za usafirishaji, usambazaji na vituo vya kupoza umeme katika Mikoa ya Dar es Salaam, Arusha na Kilimanjaro. Mradi huu ulitekelezwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kukamilika kwa mradi huu kumeimarisha upatikanaji wa umeme katika eneo la Mbagala ikilinganishwa na kipindi cha nyuma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa Kituo cha Kupoza Umeme cha Mbagala ulikamilika na kuanza kufanya kazi rasmi kuanzia tarehe 25 Februari, 2018.
• Makubaliano ya awali ya mkataba wa ujenzi wa mradi mzima ikiwemo ujenzi wa Kituo cha Kupoza Umeme cha Mbagala ulikuwa wa miezi 18 kutoka siku mkandarasi alipokabidhiwa maeneo ya ujenzi wa mradi.
• Mheshimiwa Mwenyekiti, mkandarasi amekamilisha kazi hii nje ya mkataba wa awali kutokana na kuzuiwa kufanya kazi katika baadhi ya maeneo kutokana na baadhi ya wananchi kudai kwamba hawakuridhika na fidia na hivyo kumfanya mkandarasi asikamilishe utekelezaji wa mkataba huu kwa wakati. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa hali ya umeme imeimarika katika maeneo ya Mbagala na Wizara yangu itaendelea kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi kuhakikisha hali ya umeme Mbagala inaendelea kuwa ya uhakika. Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-
Mradi wa REA Awamu ya Pili katika Jimbo la Singida Kaskazini ulisimama tangu mwaka 2016 na kukosesha huduma hiyo kwa vijiji vilivyokusudiwa mwaka 2017, utekelezaji wa REA Awamu ya Pili katika vijiji 30 kati ya 64 vilivyokusudiwa umeanza.
(a) Je, ni nini kauli ya Serikali juu ya ukamilishaji wa mradi wa REA II?
(b) Je, ni lini mkandarasi wa REA II awamu ya pili atapatikana na kuanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Mradi wa REA Awamu ya Pili katika Mkoa wa Singida ulisimama kutekelezwa mwaka 2016 kutokana na mkandarasi Spencon Ltd. kushindwa kukamilisha kazi zake baada ya kufilisika. Hata hivyo, tayari vifaa vyote vya mradi vilikuwa vimenunuliwa na kuhifadhiwa. Wakala wa Nishati Vijijini wamesaini mkataba mpya na Kampuni ya JV Emec Engineering Ltd. & Dynamic Engineering and System Co. Ltd. wenye thamani ya shilingi milioni 991.6 kwa ajili ya kukamilisha kazi za REA Awamu ya Pili katika Wilaya ya Iramba, Mkalama na Singida Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Wakala wa Nishati Vijijini umesaini mkataba na Kampuni ya JV East African Fossils Co. Ltd & CMG Construction Co. Ltd. wenye thamani ya shilingi 459.23 kwa ajili ya kukamilisha kazi katika Wilaya ya Manyoni. Mikataba yote miwili imesainiwa mwezi Machi, 2018 kwa muda wa miezi sita. Kazi ya kusambaza umeme katika meneo yaliyotajwa zitakamilika mwezi Septemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza, kazi za mradi zinatekelezwa na Mkandarasi M/S CC- Etern Consortium Ltd. ya China, kazi za Mradi wa REA III mzunguko wa kwanza katika Mkoa wa Singida zinajumuisha kuvipatia umeme vijiji 150 ambapo Jimbo la Singida Kaskazini litaunganishiwa umeme jumla ya vijiji 30 na kuunganishia wateja wa awali 870. Mradi utakamilika mwezi Juni, 2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kusambaza umeme katika Mkoa wa Singida kwa miradi ya REA awamu ya tatu mzunguko wa kwanza na wa pili zinajumuisha ujenzi wa kilometa 286.1 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33, kilometa 568 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 284 na kuunganishia wateja wa awali 8,659. Kati ya wateja hao, wateja 7,795 wa njia moja na wateja 864 wa njia tatu. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 29.56 na dola za Kimarekani milioni 5.34.
MHE. PAULINE P. GEKUL (K.n.y. MHE. JOSEPH M. MKUNDI) aliuliza:-
Je, lini Serikali itapeleka umeme katika Vijiji vya Kakerege na Nkilizya vilivyopo Nansio Ukerewe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Michael mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Nkilizya kina vitongoji saba (7) na kati ya vitongoji hivyo vitatu (3) vya Magereza, Kenonzo na Lwocho, vilipata umeme mwaka 2005 kupitia utekelezaji wa mradi wa kupeleka umeme Nansio Wilayani Ukerewe kutoka Wilaya ya Bunda ambapo wateja 60 waliunganishiwa umeme. Vitongoji viwili (2) vya Namalebe na Chamatuli vilipatiwa umeme mwaka 2012 kupitia ufadhili wa Benki ya Dunia na jumla ya wateja 47 wameunganishiwa umeme.
Mheshimiwa Spika, vitongoji vingine viwili (2) vya Mumakeke na Bubange vya Kijiji cha Nkilizya visivyokuwa na umeme, pamoja na Kijiji cha Kakerege vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea kutekelezwa kwa sasa. Kupitia utekelezaji wa mradi huu, jumla ya vijiji 35 katika Wilaya ya Ukerewe vitapatiwa umeme. Kampuni ya Nipo Group Limited aliyepewa kazi za Mradi wa REA III katika Mkoa wa Mwanza anaendelea na utekelezaji mradi huo na mradi unatarajiwa kukamilika Juni, 2019.
Mheshimiwa Spika, kazi za Mradi wa REA III Ukerewe zinajumuisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 78.32; njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 156; ufungaji wa transfoma 78 za KVA 50 na 100; pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 2,640. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 9.28.
MHE. EDWIN A. NGONYANI (K.n.y. MHE. ISSA A. MANGUNGU) aliuliza:-
a) Je, Serikali ina mpango gani wa kusambaza umeme kwenye maeneo ambayo hayamo katika miradi ya umeme vijijini, maeneo kama vile Changanyikeni, Ponde, Malela, Vikindu, Goroka A, B katika Kata ya Tuangoma na Majimatitu A, Vigozi, Machinjioni A, Mponda katika Kata ya Mianzini, Mzala, Kwa Mapunda, Kisewe, Dovya, Sai A, B katika Kata ya Chamazi?
b) Je, ni lini Serikali itamaliza tatizo la low voltage katika Jimbo la Mbagala hasa maeneo ya Kiburugwa, Kilungule, Charambe, Kijichi, Kibondemaji Chemchem na Tuangoma?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kazi ya ujenzi wa miundombinu ya kusambaza umeme katika maeneo ya Changanyikeni, Ponde, Malela, Vikindu, Goroka ‘A’ na Goroka ‘B’, Dovya Kata ya Tuangoma na maeneo ya Mponda, Vigozi, Churuvi Kata ya Mianzini ilianza Oktoba, 2017 na inatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, 2018.
Mheshimiwa Spika, kazi za mradi zinahusiana ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 12.95, njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 41.34, pamoja na ufungaji wa transfoma 19 za Kv 100 na Kv 200, gharama ya mradi ni shilingi milioni 523.84 na utekelezaji wake umefikia asilimia 90.
Mheshimiwa Spika, Jimbo la Mbagala hususan maeneo ya Kiburugwa, Kitungule, Charambe, Kijichi, Kibondemaji, Chemchem na Tuangoma kulikuwa na tatizo la uwepo wa umeme mdogo, kuanzia mwezi Juni, 2018 Serikali imechukua hatua za makusudi kuondoa tatizo hilo kwa kuboresha nguvu ya umeme kwenye maeneo hayo na hali ya umeme katika maeneo ya Mbagala imeimarika kwa kiasi kikubwa.
Mheshimiwa Spika, kukamilika kwa ujenzi wa kituo kipya cha kupoza umeme cha msongo wa kilovoti 132/33 chenye uwezo wa Mv 50 Mbagala kilichozinduliwa tarehe 22 Februari, 2018 kimeimarisha hali ya umeme katika maeneo hayo. Ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itafungua Ofisi za TANESCO Wilayani Kyerwa ili kuwafikishia karibu wananchi huduma zitolewazo na TANESCO, kama vile kununua umeme, kubadilisha mita na huduma nyingine?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika hatua ya kuboresha huduma kwa wateja Shirika la Umeme nchini (TANESCO) kupitia bajeti ya mwaka 2018/2019 inajenga Ofisi ya TANESCO Wilaya ya Kyerwa katika Kiwanja Na. 210 C, kilichopo eneo la Rwenkorongo. Kazi ya ujenzi wa ofisi hiyo inaendelea vizuri na inatarajia kukamika mwezi Januari, 2019.
Mheshimiwa Spika, katika hatua za muda mfupi TANESCO imefungua ofisi katika Mji wa Nkwenda, kwa ajili ya kuwahudumia wateja wakati kazi ya ujenzi wa ofisi mpya inaendelea. Kwa sasa Meneja wa TANESCO Wilaya ya Misenyi pamoja watumishi wengine watatu, wanaendelea kutoa huduma kwa wateja wa maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Kyerwa kupitia ofisi hiyo. Ahsante.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Serikali imekuwa na mpango kabambe wa kupeleka umeme vijijini:-
Je, ni lini Serikali itawapelekea umeme wananchi wa Kata Itandula, Nyololo Shuleni, Maduma, Udumka, Kilolo, Kiyowole na Idete?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza kuanzia Julai, 2017 hadi Juni 2019. Katika Wilaya ya Mufindi jumla ya vijiji 53 vitapatiwa umeme kupitia mradi huu unaotekelezwa na mkandarasi Kampuni ya Sengerema Engineering Group Limited aliyepewa kazi za mradi huo kwa Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Mufindi Kusini, mradi utapeleka umeme katika Kata za Makungu, Igowole, Mninga, Nyololo, Isalavanu, Mbalamaziwa na Kasanga ambapo Vijiji vya Lugolofu, Mukungu, Lugema, Ibatu, Kisasa, Makalala, Ikwega, Itulituli, Lwing’ulo, Njojo, Nyololo Shuleni, Mjimwema, Idetero, Kimandwete, Ukemele, Udumuka, Lyang’a, Kilolo, Ihomasa pamoja na Maduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za mradi katika Wilaya ya Mufindi zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 139.63, njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 170, ufungaji wa transfoma 85 za kVA 50 na 100, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 2,596. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 11.92. Kwa sasa mkandarasi ameshasimika nguzo za umeme wa line kubwa za HT kwa asilimia 90 na nguzo za umeme wa line ndogo LV kwa asilimia 95 kwa jimbo la Mufindi Kusini. Kazi ya ufungaji transfoma na kuunganisha wateja itaanza mwishoni mwa Septemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vingine vya Kata ya Itandula, Kiyowole na Idete vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa mradi wa REA III unaotarajia kuanza Julai, 2019 na kukamilika Juni, 2021. Ahsante.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI aliuliza:-
Kata za Gare, Kwai, Kwemashai, Makanya, Kilole, Ngwelo na Ubiri hazikufikiwa na REA III mpaka sasa:- Je, ni lini sasa Serikali itafikisha umeme kwenye kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Alhaji Shaabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatekeleza Miradi ya Kupeleka Miradi ya Umeme Vijijini kupitia Wakala wa Nishati (REA). Mradi wa REA III mzunguko wa kwanza ulianza Julai, 2017. Vijiji vitakavyopelekewa umeme kwenye Jimbo la Lushoto ni pamoja na Magamba, Kwegole, Kwehungulu, Kwebarabara, Maboi, Milemeleni, Kungului, Shume A, Makunguru, Shume B, Ngazi, Mhezi, Kwezindo, Kweboi, Nkelei, Viti, Langoni B, Vuli A na Kwemakulo, Mradi huu unatarajiwa kukamilika Juni, 2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya mradi huu zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 5.67, njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 46, ufungaji wa transfoma 23 za 50 kVA pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 520. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 1.9.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Kata ya Gare, Kwai, Kwemashai, Makanya, Kilole, Ngwelo na Ubiri vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa mradi wa REA III utakaoanza Julai, 2019 na kukamilika Juni, 2021. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Je, ni lini tatizo la kukatika mara kwa mara kwa umeme katika Mkoa wa Mtwara litaisha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara katika Mikoa ya Mtwara na Lindi inayopata umeme katika kituo cha kuzalisha umeme kutumia gesi asilia kilichopo Mkoani Mtwara kulitokana na kuharibika kwa mitambo ya kuzalishai umeme iliyochangiwa na uchakavu wa mitambo hiyo pamoja na urefu wa miundombinu ya kusambaza umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) imechukua hatua mbalimbali ili kutatua tatizo la kukatika kwa umeme katika mikoa hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua hizo ni pamoja na kutekeleza mradi wa ujenzi wa vituo viwili vya kukuza na kupoza umeme vyenye uwezo wa 132/33KV na 20MVA vilivyopo Mtwara Mjini na Mahumbika Mkoani Lindi, pamoja na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolt 132 ya umbali wa kilomita 80 kutoka Mtwara hadi Mahumbika. Mradi huu umekamilika na umeanza kufanya kazi rasmi mwezi Mei, 2018 na gharama ya mradi ni shilingi bilioni 16.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO imekamilisha ukarabati wa mitambo minane na mtambo mmoja uliosalia, Mzabuni wa Kampuni ya MANTRAC anaendelea na kazi ya kukarabati na inatarajia kukamilika mwezi Juni, 2018. Ili kukabiliana na ongezeko la mahitaji ya umeme katika Mikoa ya Mtwara na Lindi, TANESCO imenunua generator mbili zenye uwezo wa kufua umeme wa megawatts 4 na kazi ya kufunga mitambo hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua nyingine Mikoa ya Lindi na Mtwara imeunganishwa na Gridi ya Taifa kupitia njia ya umeme ya kilovolti 33 ambapo Mikoa hiyo sasa inapata umeme kutoka kituo cha kuppoza umeme cha Mbagala na hatua hii imeimarisha hali ya upatikanaji wa umeme na hivyo kukipunguzia mzigo kituo cha kuzalisha umeme cha Mtwara.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-
Serikali iliahidi vijiji vingi vya Jimbo la Mbulu Vijijini umeme wa REA III.
Je, ni lini sasa umeme utafika katika vijiji vya Endahargadat, Endahagichani, Qamtananat, Mewadan, Endalat, Gidbiyo na Manghay?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ya Serikali ni kufikisha umeme katika vijiji vyote Tanzania Bara visivyokuwa na miundombinu ya umeme ifikapo mwezi Juni, 2021. Jimbo la Mbulu vijijini lina vijiji vipatavyo 76, kati ya vijiji hivyo 12 vimepatiwa umeme. Vijiji 13 vya Qaloda, Getesh, Endesh, Labay, Maretadu, Hayderer, Endanachan (Haydom), Muslur, Dirim, Simha, Yaeda Ampa, Endoji na Gidhim vimejumuishwa katika mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa kwanza. Mkandarasi Kampuni ya Angelique International Limited kutoka India ameshaanza utekelezaji wa mradi na anatarajia kukamilisha kazi hiyo mwezi Juni, 2019. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa kilometa 45.87 za njia ya umeme wa msongo wa Kilovolt 33 na kilometa 35 za nja ya umeme wa msongo wa 0.4 kilovolt, ufungaji wa transfoma 16 na uunganishwaji wa wateja wa awali 347. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 2.6. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vilivyobaki vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili utakaoanza kutekelezwa Julai, 2019 hadi mwezi Juni, 2021. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:-
Lengo la Serikali ni kuhakikisha kila kijiji kinapata umeme wa REA; je, ni lini sasa vijiji vyote vya Jimbo la Busanda vitapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lolesia Jeremiah Bukwimba, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Busanda lina jumla ya Kata 22 na vijiji 83 ambapo kati ya hivyo 14 vimepatiwa nishati ya umeme; vijiji nane vitapata umeme kupitia mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa kwanza ambapo vijiji vya Bugogo, Ntono, Ihega, Butobela na Ngula ni miongoni wa vijiji vitakavyonufaika na mradi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkandarasi wa Kampuni ya White City International Contractors Electrical Power Engineering Co. Ltd ameshaanza utekelezaji wa kazi za mradi na kazi hiyo itakamilika mwezi Juni, 2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme katika Jimbo la Busanda, itajumuisha ujenzi wa kilometa 21.44 za njia ya umeme wa msongo kilovoti 33 na kilometa 26 za njia ya umeme wa msongo 0.4 kilovoti, ufungaji wa transfoma 14 na uunganishaji wa wateja wa awali 404. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 1.56.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, vijiji vitano vya Buyagu, Nyalwanzaja, Kamena, Nderema na Imalampaka vitapata umeme kupitia mradi wa ujenzi wa njia ya msongo wa 220KV wa Bulyanhulu – Geita ambapo Mkandarasi anatarajiwa kufika site mwezi Mei, 2018. vijiji 56 vilivyobaki vitapata umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu, mzunguko wa pili unaotegemewa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA aliuliza:-
Kampuni ya Utafiti wa Gesi na Mafuta imeanza kazi kubwa ya utafiti wa mafuta na gesi katika eneo la Mng’ongo, Kijiji cha Fukayosi, Kata ya Fukayosi, Wilaya ya Bagamoyo:- Je, ni nini matokeo ya utafiti huo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Shukuru Jumanne Kawambwa, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kampuni ya Gesi na Mafuta iitwayo Dodsal Hydrocarbons & Power (Tanzania) kutoka Falme za Kiarabu inaendelea na utafiti wa mafuta na gesi katika eneo la Mng’ongo katika Kijiji cha Fukayosi, Kata ya Fukayosi, Wilaya ya Bagamoyo.
Mheshimiwa Spika, kupitia utafiti huo, Kampuni ya Dodsal Hydrocarbons & Power ilifanikisha kuchimba kisima cha utafiti chenye urefu wa mita 3,866 kiitwacho Mtini-1. Kisima hicho kilianza kuchimbwa tarehe 8 Mei, 2015 na kufungwa tarehe 20 Julai 2015. Matokeo ya utafiti katika kisima hiki ni kwamba haikugundulika gesi ya kutosha kukidhi matakwa ya kiuchumi ingawaje kuna viashiria vya gesi kidogo vilivyoonekana wakati wa uchimbaji katika mashapo ya miamba ya eneo hilo. Ahsante sana.
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI aliuliza:-
Wananchi wa Kagera wana tatizo la umeme na umeme wa REA II umeingia katika center za vijiji tu.
Je, ni lini wananchi hao watapatiwa umeme ili waondokane na adha ya kutumia vibatari?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Alfredina Aporinary Kahigi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, awamu ya pili ya utekelezaji wa miradi ya kusambaza umeme vijijini ililenga pamoja na mambo mengine kufikisha umeme katika maeneo ya njia kuu, baadhi ya maeneo muhimu katika vijiji na katika taasisi za umma. Utekelezaji wa miradi ya REA Awamu ya Pili ulikamilika mwezi Desemba, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ilianza kutekeleza Mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza tangu mwezi Julai, 2017. Katika Mkoa wa Kagera vijiji vipatavyo 141 vinatarajia kupatiwa umeme kupitia mradi huu. Mradi huu utakamilika mwezi Juni, 2019. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi inahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 299, njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 574, ufungaji wa transfoma 287 za KVA 50 na 100 pamoja na kuunganishia umeme wateja wa awali 9,136. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 38.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwezi Aprili, 2018 mkandarasi Kampuni ya Nakuroi Investment Ltd. aliyepewa kazi ya ujenzi wa miundombinu ya kusambaza umeme katika Wilaya zote za Mkoa wa Kagera alikuwa ameshakamilisha kazi ya upimaji wa maeneo yatakayopelekewa umeme. Kazi zinazofanyika sasa ni kusambaza nguzo katika maeneo ya mradi na kujenga miundombinu, pamoja na kusambaza umeme.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE aliuliza:-
Katika Bunge lililopita la 2010 – 2015 Serikali iliongelea kuhusu mpango wa kuwekeza umeme unaotumia chemchemi ya maji ya moto yanayopatikana katika Kata ta Maji Moto:-
a) Je, mpango huo umefikia wapi?
b) Je, ni lini sasa Jimbo la Kavuu litapata umeme kwa maendeleo ya wananchi wa eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pudenciana Wilfred Kikwembe, Mbunge wa Kavuu, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Katavi ni moja ya mikoa inayopitiwa na Bonde la Ufa la Afrika Mashariki, hivyo kuwepo na uwezekano wa kuwa na hifadhi kubwa ya joto ardhi. Serikali inaendelea kufanya tathmini ya rasilimali ya nishati ya joto ardhi ili kujiridhisha na uwepo wa rasilimali ya kutosha kabla ya kuchoronga visima vya majaribio. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali kupitia Tanzania Geothermal Development Company imepanga kufanya utafiti wa kina katika maeneo zaidi ya 50 yenye viashiria vya joto ardhi likiwemo eneo la Maji Moto.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Jimbo la Kavuu vya Kibaoni, Usevya, Ilalangulu na Manga, vinapata umeme kutoka Sumbawanga, Mkoani Rukwa kupitia Mji wa Namanyere, Wilayani Nkasi. Aidha, vijiji vingine vya Jimbo la Kavuu ikiwa ni pamoja na Maji Moto, Mbende, Chamalangi, Mkwajuni, Ikuba, Mamba na Kasansa vitapatiwa umeme kupitia mzunguko wa kwanza wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA).
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kupatikana kwa suluhisho la kudumu la umeme katika Jimbo la Kavuu, Serikali imeanza hatua za awali za utekelezaji wa mradi wa kusafirisha umeme wa gridi, kV 400 kutoka Mbeya – Sumbawanga – Mpanda – Kigoma hadi Nyakanazi. Ujenzi wa mradi huu unatarajiwa kuanza Machi, 2019 na kukamilika mwaka 2021. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. SEIF K.S. GULAMALI aliuliza:-
Je, ni lini utekelezaji wa usambazaji wa umeme katika Kata za Igoweko, Uswaya, Tambarale, Mwisi, Sungwizi, Mwamala, Ntobo, Ngulu, Mwashiku na Kitangiri utaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Gulamali, Mbunge wa Manonga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa usambazaji wa umeme katika Kata za Igoweko, Uswaya, Tambarale, Mwisi, Sungwizi, Mwamala, Ntobo, Ngulu, Mwashiku na Kitangiri utafanyika kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza wa kusambaza umeme vijijini iliyoanza mwezi Julai, 2017 na kukamilika Juni, 2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kusambaza umeme katika kata hizi inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 zenye urefu wa kilomita 76.48; njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 60.62; ufungaji wa transfoma 36 za KVA 50 pamoja na kuunganisha wateja wa awali 733. Gharama ya kazi hii ni shilingi bilioni 1.22. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. ALBERT O. NTABALIBA aliuliza:-
Utekelezaji wa mradi wa umeme wa REA Wilayani Buhigwe unasuasua sana.
Je, ni lini vijiji vyote na vitongoji vyake pamoja na taasisi za umma zitapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Albert Obama Ntabaliba, Mbunge wa Buhigwe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Buhigwe ina kata 20, vijiji 44 na vitongoji 190. Kupitia Miradi ya REA Awamu ya Pili vijiji 14 vilipatiwa umeme, vijiji hivyo ni Kasumo, Kalege, Nyanga, Biharu, Kigege, Bulimanyi, Nyamugali, Songambele, Kavomo, Buhigwe, Mulera, Munanila, Manyovu na Mwayaya. Aidha, katika awamu hiyo taasisi mbalimbali za umma zilipatiwa umeme ikiwamo Shule ya Msingi ya Kalege, Kituo cha Afya cha Muyama, Zahanati ya Buhigwe, Kituo cha Polisi cha Buhigwe, pamoja na Ofisi ya Uhamiaji ya Munanila nayo ilipatiwa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vipatavyo 22 vya Wilaya ya Buhigwe vimejumuishwa katika Mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza unaotarajiwa kuanza kutekelezwa Mwezi Mei, 2018 katika Wilaya za Buhigwe, Kasulu, Kigoma na Uvinza. Utekelezaji wa mradi huu umechelewa kuanza katika Wilaya hizo kutokana na mmoja wa wakandarasi walioomba kazi hiyo kuilalamikia kampuni iliyokusudiwa kupewa kazi hiyo mahakamani. Vijiji vitakavyopelekewa umeme ni pamoja na Nyakimwe, Mkatanga, Rusaba, Nyaruboza, Muhinda, Kibande, Kajana, Bweranka, Kigogwe, Kibwigwa, Kinazi, Kitambuka, Munzese, Bukuba, Nyankoronko, Migongo, Mubanga, Mugera, Kirungu, Katundu, Munyegera na Nsagara. Kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa kilometa 103.64 za njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 na kilometa 142 za njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 71 na uunganishwaji wa wateja wa awali 3,011. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 8.53.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vyote na vitongoji vyake pamoja na taasisi za umma zitapelekewa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu baada ya taratibu zote zinazoendelea kukamilika. Vijiji nane vilivyobaki vitapatiwa umeme kupitia awamu ya tatu mzunguko wa pili ambao unatarajiwa kuanza Novemba, 2019 na kukamilika Juni, 2021, ahsante.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-
Katika Jimbo la Tabora Mjini hasa vijiji na kata zilizopo nje ya Manispaa ikiwemo Kata ya Tumbi na vijiji vinavyoizunguka kata hiyo havijajumuishwa katika Mpango wa REA Awamu ya Tatu.
Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA katika kata na vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Emanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli vijiji vilivyopo nje ya Manispaa ya Tabora ikiwemo Kata ya Tumbi havikujumuishwa katika utekelezaji wa mradi wa REA III mzunguko wa kwanza. Sehemu ya vijiji katika Kata ya Tumbi ilipatiwa umeme mwaka 2006 kupitia mradi wa umeme chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Sweden. Kwa kuwa baadhi ya vijiji vya Jimbo la Tabora Mjini viko ndani ya Manispaa ya Tabora, Serikali kupitia mradi wa Urban Electrification itaendelea kuyapelekea umeme maeneo yaliyomo katika Mamlaka za Miji, Manispaa na Majiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango ya Serikali ni kuipatia umeme Kata ya Tumbi na Vijiji vilivyoizunguka Kata hiyo katika Manispaa ya Tabora kupitia mradi wa Urban Electrification. Aidha, mradi wa Urban Electrification unaofadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika utepeleka umeme katika vijiji na shule za Makunga, Mkinga, Mayeye, Shalua, Mtakuja, Chang’ombe, Itetemia, Itaga na Umanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi mwingine unaotarajiwa kutekelezwa ni densification kwa nia ya kuongeza wigo wa usambazaji umeme katika vijiji ambavyo vimefikiwa na miundombinu ya umeme. Maandalizi ya awamu ya pili ya mradi huu yanaendelea na unatarajiwa kutekelezwa kwatika mwaka wa fedha 2018/2019. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO (K.n.y. MHE. CECIL D. MWAMBE) aliuliza:-
(a) Je, Serikali ina mikakati gani ya haraka kuhakikisha Vijiji vya Mumburu, Mkwera na Nanditi vinapata huduma za umeme kwani vipo karibu na nguzo kubwa za umeme?
(b) Je, Serikali itapeleka lini umeme kwenye Zahanati za Chikundi, Mbemba na Kituo cha Afya cha Chiwale?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Ndanda, lenye kipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ya Serikali ni kuvipatia umeme vijiji vyote Tanzania Bara visivyokuwa na miundombinu ya umeme ifikapo mwezi Juni, 2021. Ili kutimiza azma hiyo, Serikali imeanza kutekeleza Mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza na jumla ya vijiji vitano vimeingizwa kwenye mradi huu unaotekelezwa na Mkandarasi aitwaye JV RADI Services, Njarita Contractors and Aguila Contractors. Vijiji hivyo ni Mwambao, Mji Mwema, Nanganga B, Tuungane na Nanditi. Wigo wa kazi katika eneo hilo ni ujenzi wa kilometa 7.16 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 na kilometa 14 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4/0.23, ufungaji wa transfoma saba na kuunganisha wateja wa awali 184. Gharama za kazi hizo ni shilingi milioni 683.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Mumburu na Mkwera ni miongoni mwa vijiji 36 visivyokuwa na umeme kati ya vijiji 64 katika Jimbo la Ndanda vitakavyopatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu, mzunguko wa pili utakaotekelezwa kuanzia mwezi Julai, 2019 hadi mwezi Juni, 2021.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Zahanati ya Chikundi ina umeme tangu tarehe 25, Aprili, 2017. Aidha, Kituo cha Afya cha Chiwale kina umeme baada ya kuunganishwa wakati wa utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya Pili. Vilevile Zahanati ya Mbemba itapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza unaoendelea kutekelezwa. Ahsante.
MHE. MBARAKA K. DAU aliuliza:-
Kisiwa cha Mafia kinapata umeme kutoka kwenye jenereta kubwa ya TANESCO ambayo nayo inatumia mafuta mengi yenye gharama kubwa.
Je, ni lini Serikali itavusha umeme chini ya bahari (submarine cables) kutoka Nyamisati kwenda Kilindoni takribani kilometa 50?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau, Mbunge wa Mafia, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imefanya tafiti za awali za kuona njia bora ya kuipatia Wilaya ya Mafia umeme wa uhakika na wa bei nafuu. Tafiti za awali zilizofanyika ni kuvusha umeme chini ya bahari (submarine cables) kutoka Nyamisati hadi Kilindoni na utafiti wa pili ni kuzalisha umeme kwa kutumia vyanzo mchanganyiko (hybrid) vya umeme jua, upepo na mafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti hizi za awali zimeonesha kuwa gharama za kuzalisha umeme kwa kutumia vyanzo mchanganyiko ni nafuu zaidi na hivyo hatua za awali za utekelezaji wa mradi huu zimeshaanza. Uwezo wa mitambo hii ya kuzalisha umeme itakapokamilika inatarajiwa kuwa na megawati saba ikilinganishwa na uwezo wa megawati 3.68 zilizopo kwa sasa (megawati 2.18 zinamilikiwa na TANESCO na megawati 1.5 zinamilikiwa na kampuni binafsi ya Ng’omeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tayari TANESCO imeshapata eneo la mradi Wilayani Mafia kwa ajili ya kujenga mitambo ya kuzalisha umeme na inakamilisha taratibu za kumpata mshauri elekezi kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu utakaoainisha gharama halisi za utekelezaji wa mradi huo ambapo unatarajiwa kuanza kazi mwezi Juni, 2018 na kukamilika ndani ya miezi saba. Aidha, Benki ya Maendeleo ya Ufaransa imeonesha nia ya kufadhili mradi huo mara upembuzi yakinifu utakapokamilika.
MHE. PROF. JUMANNE A. MAGHEMBE aliuliza:-

Awamu ya III ya REA ilizinduliwa Wilayani Mwanga mnamo Julai, 2017 lakini hadi sasa utekelezaji wake haujaanza;

Je ni lini utekelezaji wa mradi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Jumanne Abdallah Maghembe, Mbunge wa Mwanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme vijijini katika Wilaya ya Mwanga kupitia REA awamu ya tatu ulianza mwezi Oktoba, 2017 ukifanywa na Mkandarasi Kampuni ya Urban and Rural Engineering Service Limited. Katika mzunguzuko wa kwanza vijiji 14 vya Wilaya ya Mwanga vitapatiwa umeme vikiwemo Vijiji vya Ndorwe, Kinghare, Kigoningoni, Kiriche, Mangulai, Kirya, Lungurumo, Mangara, Kiverenge, Kichwa, Chang’ombe, Vuchama Ngofi na Ngujini.

Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme katika Vijiji vya Wilaya ya Mwanga inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 10.98, njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 24, ufungaji wa transfoma 12 za KVA 50 pamoja na kuwaunganisha wateja wa awali 347. Kwa sasa mkandarasi anaendelea na kazi za awali ikiwemo uchimbaji wa mashimo na kusimika nguzo katika Kata ya Kirya. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivyo itakamilika mwezi Juni, 2019. Gharama ya mradi ni Sh.1,350,000,000.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:-

Halmashauri ya Busokelo ina maporomoko ya maji (waterfalls) maeneo mbalimbali na jotoardhi (geothermal):-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutumia maporomoko hayo ya maji (waterfalls) na jotoardhi (geothermal) kuweza kuzalisha umeme ili kupunguza changamoto ya umeme nchini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fredy Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika Halmashauri ya Busokelo kuna maeneo yenye maporomoko ya maji yanayoungana na maporomoko yaliyoko Wilaya ya Makete katika Mto Rumakali. Upembuzi yakinifu katika maeneo hayo ulifanywa na Serikali mwaka 1998 kwa ushirikiano na Serikali za Norway na Sweden.

Mheshimiwa Spika, kulingana na upembuzi yakinifu huo maporomoko ya Mto Rumakali yanaweza kuzalisha umeme wa MW 222. Kwa sasa TANESCO inaendelea na kazi ya kuhuisha upembuzi yakinifu kupitia ufadhili wa Benki ya Dunia kabla ya kuanza hatua za utekelezaji. Utekelezaji wa mradi utaanza Aprili, 2020 na kukamilika Desemba, 2023.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya jotoardhi ya Ngozi, Kiejo-Mbaka Mkoani Mbeya na Songwe Mkoani Songwe. Miradi hii yote imefikia hatua ya uchorongaji visima vya majaribio ili kuhakiki kiasi na ubora wa rasilimali ya jotoardhi katika maeneo hayo. Aidha, TANESCO kupitia Kampuni Tanzu ya Jotoardhi inaendelea na utafiti wa vyanzo vya umeme wa jotoardhi katika eneo la Mbaka katika Halmashauri ya Busokelo.

Mheshimiwa Spika, matokeo ya utafiti huo yataonyesha hali halisi ya uwezo wa kuzalisha umeme kwa nguvu za jotoardhi itakayopatikana katika eneo husika. Kazi ya utafiti na uchorongaji huo inatarajiwa kukamilika mwaka 2022.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-

Serikali iliahidi kuanza utekelezaji wa mradi wa umeme wa ujazo (Densification) Mkoani Geita kuanzia mwezi Oktoba, 2018 lakini hadi sasa mradi huo haujaanza:-

Je, ni lini mradi huo utaanza kutekelezwa katika Wilaya ya Mbogwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya tatu ya mradi kabambe ya kusambaza umeme vijijini unahusisha mradi wa ujazilizi (Densification) kwa kuongeza wigo wa usambazaji umeme katika vijiji ambavyo vimeshafikishiwa umeme lakini baadhi ya Vitongoji havijafikiwa na umeme. Mradi wa Grid Extension unahusu kupeleka umeme katika vijiji ambavyo havijafikiwa na miundombinu ya umeme na mradi wa Off- Grid electrification wa kuendeleza na kusambaza nishati jadidifu katika maeneo yaliyo mbali na Grid ikiwa ni pamoja na visiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilikamilisha kupeleka umeme katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi wa ujazilizi mwezi Septemba, 2018 katika awamu hiyo Vijiji na Vitongoji 305 vya Mikoa ya Arusha, Iringa, Mara, Mbeya, Njomba, Pwani, Tanga na Songwe ambapo jumla ya wateja 29,950 wameunganishiwa umeme na gharama ya mradi ilikuwa ni shilingi bilioni 68.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya pili ya mradi ya ujazilizi utapeleka umeme katika mikoa 26 Tanzania Bara katika Vitongoji 1,103 vikiwemo Vitongoji vya Wilaya ya Mbogwe kwa kuunganishia umeme wateja wa awali 69,079. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 197.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa mradi utaanza mwezi Machi, 2019 kwa muda wa miezi 12.
MHE. JOSEPH L. HAULE aliuliza:-

Jimbo la Mikumi linaitwa Jimbo la giza kutokana na kata zake nyingi kutokuwa na umeme, kama Kata ya Ulaya, Zombo, Tindiga, Mhenda, Kilangali, Vidunda na kadhalika:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Jimbo hilo ambalo limebarikiwa kuwa na Mbuga za Wanyama na vivutio kadha wa kadha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Leonard Haule, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Mikumi lina vijiji 57, kati ya vijiji hivyo vijiji 16 vina umeme. Katika utekelezaji wa azma ya Serikali ya kufikisha umeme katika vijiji vyote nchini ifikapo mwaka 2021, vijiji 41 ambavyo havijafikiwa na umeme katika Jimbo la Mikumi vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu unaoendelea sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika Jimbo la Mikumi kwa sasa inafanyika katika vijiji nane vya Ihombwe, Kwalukwambe, Vidunda, Madizini, Zombolumbo, Malui, Udung’hu na Kigunga. Kazi za kupeleka umeme katika vijiji hivyo vinahusisha ujenzi wa kilomita 26 za njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 na kilometa 32 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 16 na kuunganishia umeme wateja wa awali 533 na gharama za mradi ni shilingi bilioni mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi wa REA Awamu ya Tatu, mzunguko wa kwanza katika Jimbo la Mikumi pamoja na Mkoa wa Morogoro kwa ujumla ulianza mwezi Julai, 2018 ambapo Kampuni ya State Grid Electical and Technical Works Ltd. inatarajia kukamilisha kazi hizo mwezi Juni, 2019. Vijiji vilivyobaki 33 vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa Mradi wa REA Awamu ya Tatu unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2020/2021.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-

Serikali imeweka zuio la kusafirisha shaba ghafi kabla ya kuchakatwa, jambo ambalo limesababisha uchimbaji mdogo wa Mbesa wa Shaba usimame na wachimbaji wadogo kukosa kazi za kufanya:-

Je, ni lini Serikali itajenga mtambo wa kuchenjua shaba katika Kijiji cha Mbesa?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa tarehe 3 Machi, 2017, Serikali iliweka zuio la kusafirisha nje ya nchi madini ghafi na kuelekeza madini yote yanayoongezewa thamani yaongezewe thamani hapa nchini. Zuio hilo lilikuwa na nia njema ya kutaka shughuli zote za uongezaji thamani madini zifanyike hapa nchini ili kuongeza manufaa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla kutokana na rasilimali ya madini.

Mheshimiwa Spika, kutokana na zuio hilo, kuna GN Na. 60 ya mwaka huu, yaani tarehe 25, Januari, 2019, Serikali imetoa mwongozo wa kuhakiki uongezaji thamani madini au miamba nchini kabla ya madini hayo kupata kibali cha kusafirishwa kwenda nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, madini ya shaba yanapatikana katika maeneo mbalimbali nchini. Hivyo, kwa kuzingatia hilo, Serikali imepokea maombi ya kampuni 11 zenye nia ya kujenga vinu vya kuyeyusha madini hayo (smelters) baada ya kutangaza uwepo wa fursa hiyo. Serikali ipo katika hatua za mwisho za kuteua kampuni zitakazojenga smelters hizo ili kuwaondolea adha ya soko la madini hayo wachimbaji wadogo na wakubwa.
MHE. AUGUSTINO V. HOLLE aliuliza:-
Kwa muda mrefu Mkoa wa Kigoma umesubiri kuunganishwa kwenye Grid ya Taifa ya Umeme:-
Je, ni lini Serikali itaunganisha Mkoa huo kwenye Grid ya Taifa ya Umeme?
NAIBU WAZIRI NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Vuma Holle, Mbunge wa Jimbo la Kasulu Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO mwezi Desemba, 2017 ilikamilisha upembuzi yakinifu kwa ajili ya kujenga njia ya kusafirisha umeme ili kuunganisha Mkoa wa Kigoma na Grid ya Taifa kutokea Tabora. Mradi unahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Kidahwe Mkoani Kigoma kupitia Urambo na Nguruka umbali wa kilomita 370. Kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa vituo vya kupozea umeme vya 132/33 KV katika Miji ya Urambo na Nguruka. Gharama ya kazi hizo inakadiriwa kufikia Dola za Marekani 81,000,000 na ujenzi wa mradi unatarajia kuanza mwezi Machi, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2020.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa upande mwingine inatekeleza ujenzi wa mradi wa kusafisha umeme…
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa upande mwingine inatekeleza ujenzi wa mradi wa kusafisha umeme wa North West Grid KV 400 Mbeya – Tunduma – Sumbawanga – Mpanda – Kigoma – Nyakanazi wenye urefu wa kilometa 1372. Mradi huu utawezesha kuyaunganisha maeneo ya Magharibi na Kaskazini Magharibi mwa Tanzania katika Grid ya Taifa na kuondoa matumizi ya mitambo ya mafuta katika maeneo hayo. Kwa sasa mikataba ya makubaliano ya fedha imesainiwa kati ya Tanzania na Benki ya Dunia pamoja na Benki ya Maendeleo ya Afrika na mradi utagharimu Dola za Kimarekani 455,000,000.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia imeanza utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa MW 45 kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Malagarasi. Ujenzi wa mradi huo utaenda sambamba ujenzi wa wa njia ya kusafirisha umeme wa mgongo wa KV 132 yenye urefu wa kilometa 53 kutoka Malagarasi hadi Kidahwe Kigoma unatarajiwa kujengwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020 na kukamilika 2020/2021.
MHE. MUSA E. NTIMIZI aliuliza:-
Katika mradi wa kupeleka umeme vijijini, Jimbo la Igalula limepitiwa na umeme katika baadhi ya maeneo ya Kata za Kigwa, Igalula, Goweko na Nsolola tu kati ya Kata kumi na moja za Jimbo hilo:-
a) Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka umeme katka Kata na Vijiji vya Jimbo la Igalula vilivyobaki?
b) Katika Kata ya Igalula, Kijiji cha Igalula ambapo kuna bwawa la maji kuna hitaji la nguzo kumi tu kwa ajili ya kusaidia kusukuma mitambo ya maji. Je, Serikali itasaidiaje kupeleka nguzo hizo ili kutatua tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Musa Rashid Ntimizi, Mbunge wa Jimbo la Igalula, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya kupeleka umeme vijijini kupitia mradi wa REA III mzunguko wa kwanza. Katika Jimbo la Igalula lililopo Wilayani yui jumla ya vijiji 98 vitanufaika na Mradi wa REA III. Kupitia mradi huu jumla ya vijiji 25 vitaunganishiwa umeme. Aidha, vijiji 73 vilivyobaki vitapatiwa umeme kupitia REA III Mzunguko wa Pili utakaoanza kutekelezwa Mwezi Julai, 2019 na kukamilika Mwezi Juni, 2021.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa mkandarasi kampuni ya Intercity Builders Limited anaendelea na kazi za ujenzi wa miundombinu ya kusambaza umeme katika vijiji vya Kata za Ibelamilundi, Ibiri, Kigwa, Goweko, Nsololo na Igalula. Aidha, vijiji vya Kigwa B, Goweko Market, Goweko Tambukareli, Goweko Juu, Imalakaseko, Igalula I na Igalula II vilipatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Pili uliokamilika mwezi Desemba, 2016.
Mheshimiwa Spika, kazi ya Mradi wa REA III unaondelea sasa katika Jimbo la Igalula zinajumuisha ujenzi wa njia ya msongo wa kilovott 33 yenye urefu wa kilometa 66.79; njia ya umeme wa msongo wa killovot 0.4 yenye urefu wa kilometa 102.242; ufungaji wa transforma 34; pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 2,235. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 6.62.
(b) Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Igalula ambako kuna bwawa la maji, TANESCO imeshakamilisha kazi na umeme umeshawashwa katika kituo cha pampu ya maji. Ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza:-

Mji wa Itigi unakua kwa kasi na umeme umeenda vijiji vya Lulanga, Itagata, Ukimbu, Chabutwa, Mtakuja, Makale na Mitundu ambapo ni kilomita 71; kwenda Itigi hadi Mwamagembe ni zaidi ya kilomita 130:-

(a) Je, Serikali haioni ni vema sasa kuipa TANESCO hadhi ya Kiwilaya katika Wilaya ya Itigi?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza watumishi wa Shirika la Umeme katika Jimbo la Manyoni Magharibi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuleta ufanisi katika kuwahudumia wananchi wa Mji wa Itigi katika Jimbo la Manyoni Magharibi mwaka 2003 TANESCO ilianzisha Ofisi ndogo ya Itigi kwa lengo la kuongeza huduma za umeme kwa wananchi. Aidha, TANESCO imekuwa ikifungua ofisi kwa ajili ya kutoa huduma kwa wateja wake katika maeneo mbalimbali nchini. Vilevile Ofisi hizo zimekuwa zikipandishwa hadhi kutoka ofisi ndogo hadi kuwa Ofisi za Wilaya na Mkoa za TANESCO kwa kuzingatia mahitaji ikiwa pamoja na kukua kwa shughuli za uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa TANESCO imefungua ofisi katika Mji wa Itigi kwa ajili ya kuwahudumia wateja katika hadhi ya ofisi ndogo. Hata hivyo, TANESCO imeanza taratibu za kupandisha ofisi hiyo hadhi ili kuwa ofisi ya TANESCO ya Kiwilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya TANESCO Itigi inasimamiwa na Techinician na watumishi wengine 11. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, TANESCO inatarajia kuongeza watumishi wengine watano pamoja na Mwandisi ili kuwahudumia wateja wa maeneo yote ya Itigi ikiwa ni pamoja na wateja kutoka Vijiji vya Lukanga, Itagata, Ukimbu, Chabutwa, Mtakigi, Makle, Mitundu na Mwamagembe.
MHE. HASNA S. K. MWILIMA aliuliza:-

Tarafa ya Nguruka ina wakazi zaidi ya 100,000 na ndio kitovu cha biashara:-

(a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kupeleka umeme wa Grid ya Taifa kutoka Usinge, Wilaya ya Kaliua?

(b) Wakazi wa Kata za Mwambao, Sunuka, Kaliya, Buhigu, Igalula, Haramba na Sigunga hawana umeme na Jiografia ya kuwaunganishia umeme kutoka Uvinza ni ngumu. Je, Serikali haioni umuhimu wa kupeleka umeme kutoka Mpanda, Mwese kwenda Kata ya Kaliye, ili iwe rahisi kuzipitia kata zingine?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hasna Sudi Katunda Mwilima, Mbunge wa Kigoma Kusini, lenye Sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanza kutekeleza mradi wa kusafirisha umeme mkubwa wa kilovoti 400 katika Mikoa ya Kusini Magharibi, ikiwemo Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma kwa lengo la kuwaunganisha wananchi wa maeneo hayo na Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua za awali Serikali kupitia TANESCO kwa kushirikiana na Benki ya Dunia na Benki ya Maendeleo ya Afrika imeanza kutekeleza mradi wa njia ya kusafirisha umeme mkubwa wa kilovoti 400 North West Grid Kv 400, Iringa – Mbeya – Tunduma – Sumbawanga
– Mpanda – Kigoma – Nyakanazi wenye urefu wa kilometa 1,372. Kwa sasa Benki ya Dunia imeshatoa dola za Kimarekani milioni 455 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na utekelezaji wa mradi huu Serikali kupitia TANESCO mwezi Disemba, 2018 imeanza kutekeleza mradi wa kuunganisha Mkoa wa Kigoma na Grid ya Taifa kutoka Mkoa wa Tabora. Mradi unahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora, Urambo, Usinge – Kaliua, Nguruka hadi Kidahwe Kigoma Mjini wenye urefu wa kilometa 370. Kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa vituo vya kupoza umeme vya 132/33 Kv katika Miji ya Urambo na Nguruka. Gharama ya kazi hiyo inakadiriwa kufikia dola za kimarekani milioni 81 na ujenzi wa mradi unatarajiwa kukamilika mwezi Februari, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa mradi huu na miradi mingine inayoendelea kutaimarisha upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Kigoma ikiwa ni pamoja na kuwasambazia wananchi umeme katika Kata za Mwambao, Sunuka, Kaliya, Buhigu, Igalula, Haramba na Sigunga. Nakushukuru.
MHE. GODBLESS J. LEMA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kunufaika na nishati mbadala itokanayo na jua hasa, katika mikoa yenye ukame unaosababishwa na jua kali kwa kutengeneza Solar Village na kuunganisha nishati hiyo kwenye Gridi ya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godbless Jonathan Lema, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO inatekeleza Mradi wa Nishati Endelevu kwa Wote (Sustainable Energy for all – SE4ALL) chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).

Kazi zilizofanyika hadi kufikia Disemba, 2018 ni pamoja na uhakiki wa kubainisha sehemu zinazofaa kwa uzalishaji wa nishati ya umeme-jua katika maeneo ya Same (Kilimanjaro) Zuzu (Dodoma) na Manyoni (Singida). Ili kuwa na uhakika wa uwezo wa kuzalisha umeme katika maeneo hayo, Serikali kupitia TANESCO imeanza kufanya upembuzi yakinifu katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO imeanza kutekeleza mradi wa kuzalisha umeme-jua wa MW 150 katika Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga. Gharama ya mradi ni Dola za Marekani milioni 375.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mshauri Mwelekezi anatarajia kukamilisha upembuzi yakinifu mwezi Machi, 2019. Ujenzi wa mradi unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2019 na kukamilika mwezi Machi, 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na utekelezaji wa miradi hii, Serikali kupitia TANESCO mwezi Oktoba, 2018, ilitangaza zabuni kwa ajili ya kupata wawekezaji binafsi watakaozalisha umeme. Kampuni 52 zimeonesha nia ya kuzalisha umeme kutoka chanzo hicho na hivi sasa, TANESCO wanafanya uchambuzi kwa ajili ya kupata Kampuni ya kuzalisha umeme MW 150 kutoka vyanzo mbalimbali vya nishati jadidifu pamoja na umeme wa jua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. LUCY S. MAGERELI aliuliza:-

Wilaya ya Kigamboni inakabiliwa na tatizo la msongo mdogo wa umeme na matukio ya kukatika umeme ya mara kwa mara hata mara tatu kwa siku:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukomesha tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Simon Magereli, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na tatizo la umeme kupungua nguvu (low voltage) katika maeneo ya Manispaa ya Mji wa Kigamboni kutokana na uchakavu wa mifumo ya umeme pamoja na kuongezeka kwa mahitaji ya umeme kutokana na kasi ya ujenzi wa nyumba za makazi na viwanda. Serikali kupitia TANESCO inaendelea na kazi ya kuboresha hali ya umeme (voltage improvement) kwa kuongeza njia za umeme na transformer katika maeneo ya Kigamboni yakiwemo Vijibweni, Kibugumo, Kibada, Uvumba, Kisota, Maweni na Kwa Thoma.

Katika kushughulikia tatizo hili, Serikali kupitia TANESCO mwaka 2017 ilifanya matengenezo kwa ajili ya kuboresha Kituo cha Kupooza Umeme Kigamboni kwa kukiongezea uwezo wake kutoka MVA 5 iliyokuwa inahudumia wateja 3000 kufikia MVA 15 yenye uwezo wa kuhudumia wateja 12,000. gharama ya mradi ni shilingi 1,500,000,000/=.

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha ujenzi wa Kituo Kipya cha Kupooza Umeme cha Kurasini cha 132/33KV kitakachopeleka umeme wa uhakika katika maeneo ya Kigamboni. Ujenzi wa kituo hicho ulianza mwaka 2018 na utakamilika mapema mwezi Aprili, 2019 na hivyo kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme Kigamboni.

Mheshimiwa Spika, katika hatua nyingine Serikali kupitia TANESCO inaendelea na kazi ya ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 132 kutoka Kurasini hadi Dege na ujenzi wa kituo kipya cha kupoza umeme cha MVA 120 katika eneo la Dege Kigamboni. Mradi huu ulianza kutekelezwa kuanzia mwezi Januari, 2018 kwa gharama ya shilingi bilioni 16 na utakamilika ifikapo Septemba, 2019. Kukamilika kwa mradi huu kutaimarisha na kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme katika maeneo ya Mbagala na Kigamboni na hivyo kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo la kukatika umeme kwa Wilaya za Kigamboni na Temeke. Ahsante.
MHE. ZAYNABU M. VULU (Kn.y. MHE. ALLY S. UNGANDO) aliuliza:-

Ukarabati wa Kituo cha Afya Mbwera yakiwemo majengo ya upasuaji, Wodi ya Wazazi na mengineyo unakwenda kwa kasi sana:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka umeme kwenye Kituo cha Afya Mbwera?

(b) Je, ni lini kazi hiyo itaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Seif Ungando, Mbunge wa Kibiti, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali itapeleka umeme katika Vijiji vya Mbuchi, Mbwera Mashariki na Mbwera Magharibi kupitia utekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini (REA) III unaoendelea. Kazi hiyo itaanza Mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021. Mradi huo unahusisha kupeleka umeme wa Gridi ya Taifa katika eneo la Mbwera kutoka Muhoro kwa kujenga njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 40; ujenzi wa njia ya kusambaza umeme yenye urefu wa kilomira 2.78; ufungaji wa transfoma moja (1) ya KVA 50; pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 48 ikiwemo Kituo cha Afya cha Mbwera. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 1.56. Ahsante.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO (K.n.y. MHE. PROF. NORMAN A. SIGALLA KING) aliuliza:-

Kumekuwa na maandalizi ya kuzalisha umeme katika Mto Lumakali uliopo Balogwa Makete na ni miaka 11 sasa wananchi wanaendelea kusubiri ambapo mwaka 2015/2016 Serikali ilitoa kauli kwamba ujenzi huo ungeanza mwaka 2017.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga bwawa hilo kwa ajili ya kuzalisha umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Norman Adamson Sigalla, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa kuzalisha umeme katika mto Lumakali unahusisha ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme wa MW 222 na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa Kilovoti 220 kutoka eneo patakapojengwa mitambo ya kuzalisha umeme Lumakali hadi Kituo cha Kupooza umeme cha Mbeya. Jumla ya gharama za mradi inakadiliwa kuwa Dola za Marekani milioni 388.22.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Lumakali ulifanyiwa upembuzi yakinifu mwaka 1998. Kwa sasa Mshauri Mwelekezi wa Mradi anakamilisha mapitio ili kuboresha Upembuzi Yakinifu uliofanyika mwaka 1998 na kazi hiyo itakamilika Mwezi Machi, 2020. Utekelezaji wa Mradi huu utaanza Mwezi Januari, 2021 na kukamlisha mwezi Juni, 2023.
MHE. PAULINE P. GEKUL aliuliza:-

Je, ni lini wananchi wanaodai fidia ya maeneo yao yaliyopitiwa na mradi wa KV 400 katika Jimbo la Babati Mjini watalipwa.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Philip Gekul, Mbunge wa Babati Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) linatekeleza mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 400 kutoka Singida hadi Namanga kupitia Arusha. Mradi huu unahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 400 yenye urefu wa kilomita 414 na upanuzi wa vituo vya kupozea umeme vya Singida na Arusha na usambazaji wa umeme katika vijiji 14 vinavyopitiwa na mradi. Gharama za mradi huu ni Dola za Kimarekani milioni 258.82.

Mheshimiwa Naibu Spika, ulipaji fidia ulianza mwezi Agosti, 2018 baada ya kukamilika kwa zoezi la uthamini na uhakiki wa mali na mazao yatakayoathirika na utekelezaji wa mradi. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Machi, 2019 fedha zaidi ya shilingi bilioni 31.87 zimeshalipwa kwa waathirika 2,815 kutoka Wilaya za Arusha, Monduri, Babati pamoja na Hanang’.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Wilaya ya Babati, fedha zaidi ya shilingi 6,200,800,000 zimeshalipwa kwa wananchi 995 hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Machi, 2019. Wananchi 86 waliobaki watalipwa fedha zao shilingi milioni
638.18 wakati wowote baada ya kukamilika kwa zoezi la uhakiki linaloendelea.
MHE. MUHAMMED AMOUR MUHAMMED aliuliza:-

Suala la mafuta ni la Muungano na kumekuwepo na taratibu mbalimbali zinazofanywa ili kutafuta mafuta nchini:-

Je, ni taratibu zipi zilizopaswa kufanyika ili kuthibitisha kwamba mafuta yanapatikana katika eneo husika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Muhammed Amour Muhammed, Mbunge wa Bumbwini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwa mujibu wa Katiba iliyopo, suala la utafutaji na uzalishaji mafuta ghafi ni suala la Muungano. Hata hivyo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar mwaka 2015 kwa nia njema ya kuongeza ufanisi na tija katika shughuli za kutafuta na kuzalishaji mafuta ghafi, zilikubaliana kuwa kila upande usimamie shughuli hizo kwa kutumia sheria na taasisi zake. Serikali zetu za pande zote mbili za Muungano zimefanya hivyo katika masuala ya bandari na viwanja vya ndege, pamoja na kuwa masuala hayo ni ya Muungano.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuthibitisha mafuta yanapatikana katika eneo husika, taratibu zifuatazo hufanyika ikiwa ni pamoja na:

(a) Utafiti wa awali wa kukusanya sampuli za kijiolojia na kijiochemia;

(b) Kukusanya data za kijiofizikia (gravimetry na seismic);

(c) Kufanya tathmini (interpretation) ya data za kijiolojia na kijiofizikia;

(d) Kutambua maeneo ya mashapo (geological structures) katika miamba tabaka ambapo mafuta au gesi inaweza kukusanyika kufuatia matokeo ya tathmini ya data za kijiolojia na kijiofizikia; na

(e) Kuchimba visima vya utafiti (exploration wells) katika maeneo yalikotambulika mashapo ili kuthibitisha uwepo wa mafuta ghafi au gesi asilia.
MHE. UPENDO F. PENEZA (K.n.y. MHE. PETER A. LIJUALIKALI) aliuliza:-

Je, ni lini programu ya REA III itaanza kutekelezwa katika vijiji ndani ya Wilaya ya Kilombero?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Peter Ambrose Lijualikali, Mbunge wa Kilombero, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ilianza kutekeleza Mradi wa Usambazaji Umeme Vijijini ikiwemo vijiji vya Wilaya ya Kilombero Julai, 2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni ya State Grid Electrical and Technical Works Ltd Novemba, 2018 ilikamilisha upimaji na usanifu katika vijiji 21 vya REA III, Mzunguko wa Kwanza. Kwa sasa mkandarasi anaendelea na kazi ya ujenzi wa miundombinu katika Vijiji vya Kirama, Mbasa, Michenga, Mautanga, Ihanga na Miwangani. Kazi za ujenzi wa mradi huu zitakamilka mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za mradi wa Jimbo la Kilombero zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa Kilovoti 33 umbali wa kilomita 16.5, njia ya umeme wa msongo wa Kilovoti 04 urefu wa kilomita 28, ufungaji wa transformer 14 za KVA 50 na 100, pamoja na kuunganisha umeme wateja wa awali 497 na gharama ya mradi ni shilingi 1,700,060,000/=. Ahsante sana.
MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-

Mradi wa Umeme mkubwa wa msongo wa KVA 400 toka Kinyerezi kupitia Pwani, Morogoro, Singida na Arusha umechukua maeneo ya wananchi kwa muda mrefu bila kuwalipa fidia:-

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kulipa fidia hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Silyvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO inatekeleza mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa Kilovolts 400 kutoa Kinyerezi - Dar es salaam na Rufiji - Pwani kupitia Chalinze hadi Dodoma. Malengo ya mradi huo ni kuongeza upatikanaji wa umeme katika ukanda wa Mashariki, Kati na kaskazini mwa nchi kutoka kwenye mitambo ya kuzalisha umeme (Kinyerezi) na mradi wa Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya kwanza ya upimaji njia na kutathmini mali za wananchi watakaopisha mradi kutoka Kibaha hadi Chalinze ilikamilika Mwezi Desemba, 2017 na kuidhinishwa na Mthamini Mkuu wa Serikali Mwezi Novemba, 2018. Serikali kupitia TANESCO Mwezi Januari, 2019 itatangaza zabuni kwa ajili ya kumpata mtaalam mshauri wa kufanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa Kilovoti 400 kutoka Rufiji hadi Chalinze na kuhuisha upembuzi yakinifu wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 400 kutoka Kinyerezi hadi Chalinze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya shilingi bilioni 21 na milioni 600 zinatakiwa kulipwa kama fidia kwa wananchi katika maeneo ya Halmashauri za Kisarawe, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini na Chalinze na eneo la Kiluvya na taratibu zote za uandaaji taarifa na majedwali ya malipo ya fidia zimekamilika. Serikali inatarajia kutenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 34 kupitia bajeti ya mwaka wa fedha 2019/2020 kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wananchi wa maeneo hayo baada ya kukamilika kazi ya kuhuisha upembuzi yakinifu ikiwa ni pamoja na gharama za mradi wa kipande cha Kinyerezi Chalinze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba wananchi waendelee kuvuta subira wakati Serikali inaendelea kukamilisha taratibu za malipo yao ya fidia. Ahsante.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA aliuliza:-

Gesi ambayo imegunduliwa katika Mkoa wa Mtwara itanufaisha wananchi wote nchini na Taifa kwa ujumla:-

Je, Serikali ina mpango gani mahususi wa kujenga Chuo kitakachotoa mafunzo ya gesi na mafuta katika Kanda ya Kusini ili vijana wa Lindi na Mtwara na maeneo mengine waweze kupata taaluma na kuweza kushiriki kwenye sekta hii?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shamsia Aziz Mtamba, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali itaendelea kuvitumia vyuo vilivyopo nchini kuwajengea uwezo wa kitaaluma wananchi katika masuala ya utafutaji, uendelezaji, uzalishaji, uchakataji, usafirishaji na usambazaji wa mafuta na gesi asilia. Kwa mfano, kwa mwaka 2010 Kampuni ya Petrobras ilitumia Dola za Marekani 350,000 sawa na shilingi milioni 780 kufundisha na kukipatia Chuo cha VETA Mtwara vifaa vya mafunzo. Aidha, kupitia mpango huo wanafunzi 50 na wakufunzi wawili walifundishwa kwenye fani ya umeme na makanika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya Statoil imekuwa ikifadhili mafunzo mbalimbali kwa ngazi za vyuo kwa mfano mwaka 2013 ilifadhili wananchi tisa kusoma shule ya biashara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, masuala ya fedha na uchumi wamafuta na gesi asilia. Aidha, Kampuni ya BG waliendesha mafunzo na VETA Mtwara kwenye fani za English Language, Food preparation, Plumbing, Welding, Carpentry, Motor Vehicle Maintenance, Electrical Installation and Maintenance.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia iliyokuwa Wizara ya Nishati na Madini mwaka 2013 ilitoa ufadhili kwa wanafunzi 50 kusoma Chuo cha VETA Mtwara. Aidha, Serikali kupitia TPDC imefungua klabu 32 za mafuta na gesi katika shule za sekondari za mikoa ya Lindi na Mtwara kwa lengo la kutoa elimu inayohusu tasnia ya mafuta na gesi asilia pamoja namna inavyoweza kuwanufaisha kupitia fursa zinazotengenezwa na tasnia hii katika maeneo yao.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE aliuliza:-

Katika Jimbo la Mpwapwa Vijiji vya Mkanana, Nalamilo, Kiboriani, Igoji Kaskazini, Mbori, Tambi, Nana, Majani (Mwenzele), Mafuto, Kiegea, Kazania, Chimaligo, Mbugani, Chilembe, Mazaza, Mwanjili, (Makutupora) na Chibwegele havina huduma ya umeme:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuvipatia huduma ya umeme vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa George Malima Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya vijiji 31 katika Wilaya ya Mpwapwa vitapatiwa umeme kupitia Miradi ya Umeme Vijijini inayoendelea. Kupitia Mradi wa REA III Mzunguko wa Kwanza unaoendelea jumla ya vijiji 14 vitapatiwa umeme. Hadi sasa Vijiji vya Mbori, Tambi, Mnase, Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Mpwapwa, Kimangai na Chunyu Sekondari vimepatiwa umeme kupitia Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini (REA III) Mzunguko wa Kwanza unaoendelea kutekelezwa hivi sasa na mkandarasi Kampuni ya A2Z Ifra Engineering Limited kutoka nchini India. Kazi za mradi katika Wilaya ya Mpwapwa zinahusisha ujenzi wa njia za umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 9.45, njia za umeme wa msongo kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 68, ufungaji wa transfoma 34 za kVA 50 na 100, pamoja na kuunganisha umeme kwa wateja wa awali 1,148 na gharama za mradi ni shilingi bilioni 2 na milioni 600.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vilivyosalia ikiwa ni pamoja na Mkanana, Ngalamilo, Kiboriani, Nana, Majami, Mafuto, Kiegea, Kazania, Chimaligo, Mbugani, chihembe, Mazaza, Mwanjiri na Chibwegerea vitapatiwa umeme katika Mzunguko wa Pili wa Mradi wa REA III unaotarajiwa kuanza Julai, 2019 na kukamilika Juni, 2021. Ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza:-

Serikali ina mpango wa kufikia uzalishaji wa zaidi ya megawatts 5,000 za umeme ifikapo 2020.

Je, ni mkakati gani umewekwa ili kufikia lengo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athumani Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha Tanzania inajenga uchumi wa viwanda, Serikali kupitia Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015 imeweka mipango ya kuzalisha umeme wa kutosha na unaotabirika. Serikali kupitia Wizara ya Nishati imeweka mpango wa kuzalisha umeme wa megawatts 5000 ifikapo mwaka 2020. Kufutia mpango huo, Serikali inatekeleza miradi mbalimbali ya kuzalisha umeme kutokana na vyanzo mbalimbali vikiwemo maji, gesi asilia na jua. Miongoni mwa miradi ya kuzalisha umeme inayotekelezwa ni pamoja na upanuzi wa mradi wa kufua umeme kwa kutumia gesi asilia Kinyerezi I kutoka megawatts 150 za sasa na kufikia megawatts 335. Utekelezaji wake unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Agosti, 2019.

Mheshimiwa Spika, miradi mingine ya kufua umeme kwa gesi asilia ni Kinyerezi II, megawatts 240 ambao utekelezaji wake umekamilika mwezi Aprili, 2018, badala ya 2019 inayosomeka hapo na mradi wa kuzalisha umeme wa Mtwara wa megawatts 300 unaotekelezwa chini ya ufadhili wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA). Mradi huu unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Machi, 2019.

Mheshimiwa Spika, mwezi Disemba, 2018, Serikali ilianza kutekeleza mradi za kuzalisha umeme wa kutumia nguvu ya maji (Stiegler’s Gorge) megawatts 2,115 pamoja na mradi wa Rusumo, megawatts 80. Miradi mingine itakayoanza kutekelezwa hivi karibuni ni mradi wa Ruhudji, megawatts 358, mradi wa Rumakali, megawatts 222 na mradi wa Kakono, megawatts 87. Miradi hii inatarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali pia itatekeleza miradi ya kuzalisha umeme wa nguvu za jua megawatts 150 (Kishapu), upepo megawatts 100 (Singida) na miradi ya Makaa ya Mawe megawatts 600.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa miradi hii itaongeza umeme katika gridi ya Taifa kutoka megawatts 1602 kutoka kwenye vyanzo vilivyotumika kuzalisha umeme kwa sasa na kufikia megawatts 10,000 ifikapo 2025.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza:-

Je, ni lini kiwanda cha Saruji cha Dangote kitapewa gesi asilia na TPDC?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Nanyamba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petrol Nchini (TPDC) imekamilisha kazi ya ujenzi wa miundombinu ya kupeleka gesi asilia katika mitambo ya kuzalisha umeme wa muda katika Kiwanda cha Saruji cha Dangote umbali wa mita 100 kutoka katika Toleo la Kwanza la Gesi (Block Valve Station No. 1).

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya kwanza ya mradi wa kuwezesha matumizi ya gesi kuzalisha umeme kwa Kiwanda cha Dangote ilikamilika na kuanza kufanya kazi Agosti, 2018 ambapo hadi kufikia Aprili, 2019, Kiwanda cha Dangote kimeanza kutumia wastani wa futi za ujazo milioni tano kwa siku kwa kuzalisha umeme.

Awamu ya pili ya mradi inahusu ujenzi wa miundombinu ya bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka BVS 1 kwenda kwenye Kiwanda cha Dangote, umbali wa kilimita 2.7 kwa ajili ya kuwezesha gesi asilia kutumika kama nishati ya kuchoma malighafi ya kuzalisha saruji. Jumla ya gharama za mradi ni shilingi bilioni nane na milioni mia mbili. Awamu ya pili ya mradi ilikamilika Desemba, 2018 na sasa Kiwanda cha Dangote kinatumia gesi ya wastani wa futi za ujazo milioni 15 hadi 20 kwa siku kwa ajili ya uzalishaji wa saruji.
MHE. AJALI R. AKBAR aliuliza:-

Takwimu zilizopo zinaonesha kuwa gesi kutoka Mtwara na Songosongo inatumika kwa asilimia sita tu:-

(a) Je, kwa nini Kiwanda cha Saruji cha Dangote na Mtwara Cement Mkoani Mtwara havijapatiwa umeme wa gesi asilia hadi leo?

(b) Je, kwa nini Wananchi wa Mtwara wasiunganishiwe gesi asilia kwenye nyumba zao?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Ajali Akbar, Mbunge wa Newala Vijiji, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa kiwanda cha Saruji cha Dangote kimeunganishwa na miundombinu ya gesi asilia ambapo awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi wa kuwezesha matumizi ya gesi asilia kuzalisha umeme kwa ajili ya kiwanda cha Dongote ilikamilika na kuanza kufanya kazi mwezi Agosti, 2018.

Aidha, hadi kufikia Mwezi Aprili, 2019 kiwanda cha Dangote kimeanza kutumia wastani wa futi za ujazo milioni tano kwa siku kwa kuzalisha umeme. Awamu ya pili ya mradi ilikamilika mwezi, Desemba, 2018 na sasa kiwanda cha Dangote kinatumia gesi ya wastani wa futi za ujazo milioni 15 hadi milioni 20 kwa siku kwa ajili ya uzalishaji wa Saruji. Jumla ya gharama za mradi ni shilingi bilioni 8,200.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa TPDC inaendelea na utekelezaji wa mradi kwa kuagiza na kujenga miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia majumbani, viwandani na katika Taasisi mbalimbali kwa Mikoa ya Mtwara, Pwani na Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi wa kusambaza gesi asilia Mkoani Mtwara imeshaanza ambapo kwa sasa kazi ya ununuzi wa vifaa, mabomba, mita za kupimia gesi pamoja na vifaa vya kupunguza mgandamizo wa gesi inaendelea. Inategemewa zaidi ya Kaya 120 za awali zitaunganishwa mabomba ya gesi Mkoani Mtwara kwa matumizi ya nyumbani ifikapo Mwezi Juni, 2019.
MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Mapema mwaka 2016 Waziri wa Nishati alifanya uzinduzi wa Mradi wa Umeme wa REA na kuagiza Vijiji vya Sarakwa, Tingirima, Rakana, Nyang’aranga, Nyamakumbo, Saba–Osanza, Mmagunga, Nyabuzume, Bukama, Tiring’ati, Bigegu, Nyaburundu, Masaba, Nyansirori, Nyamuswa A, Saloka-Guta, Mahanga, Manchimweru, Nyangere, Makongoro A na B na Nyamuswa kupatiwa umeme:-

(a) Je, ni lini kifanyike ili miradi ya vijiji 21 ikamilike kwa wakati kama Serikali ilivyoahidi?

(b) Je, ni nani aliyepanga kijiji A kipate kilomita tatu, transfoma mbili au nguzo 20 na umeme upitie eneo bila kushirikisha vijiji na hata bila kujali wingi wa kaya?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendeelea kutekeleza mradi wa kupeleka umeme katika Vijiji vya Bunda vikiwemo vijiji 21 kupitia kampuni ya Derm Electric Company Limited. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2019, mkandarasi alishawasha umeme katika Vijiji vya Nyangere, Bukama, Mugaja Centre, Marambeka, Bunere, Shule ya Msingi Mugaja pamoja na kuunganisha umeme wateja wa awali 289.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa mkandarasi anaendelea na kazi ya kusimika nguzo, kuvuta nyaya na kufunga transfoma katika Vijiji vya Sarakwa, Tingirima, Rakana, Nyang’aranga, Nyabuzume, Tiring’ati, Bigegu, Nyaburundu, Guta B, Mahanga, Manchimweru na Makongoro A na B. Kazi za mradi wa kupeleka umeme katika vijiji hivyo inahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 74.8; njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 120; ufungaji wa transfoma 53 za KVA 50 na 100; pamoja na kuunganisha umeme kwa wateja wa awali 1,141. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 7.08 na kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi itakamilika ifikapo mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Vijiji vya Nyamakumbo, Saba – Osanza, Mmagunga, Masaba, Nyansirori na Nyamuswa vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III, mzunguko wa pili, unaotarajiwa kuanza Mwezi Julai, 2020 na kukamilika mwezi Juni, 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya upimaji hufanywa na Serikali kupitia TANESCO, REA na viongozi wa Serikali za Vijiji husika. Kipaumbele ni kupeleka umeme katika maeneo yasiyokuwa na miundombinu ya umeme na katika taasisi zinazotoa huduma za kijamii kama vile vituo vya afya, zahanati, shule na kadhalika. Hata hivyo, ukubwa wa wigo wa mradi wa usambazaji umeme katika mkoa, wilaya na kijiji husika hutegemea zaidi upatikanaji wa fedha.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-

Jimbo la Tunduru Kusini lina jumla ya vijiji 65, kati ya hivyo ni vijiji vinne tu ndiyo vimefikiwa na umeme wa REA Awamu ya I na ya II:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA katika vijiji 61 vilivyobaki?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Idd Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza miradi ya kusambaza umeme katika vijiji vyote nchini. Jimbo la Tunduru Kusini lina vijiji 65, kati ya vijiji hivyo Vijiji vinne vya Azimio, Chiwana, Mkandu na Mbesa ndivyo vimekwishapata umeme kupitia mradi wa REA II na Vijiji vingine vinne vya Mchuluka, Umoja, Masalau na Msinji vinatarajiwa kupatiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea na unaotegemea kukamilika mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme katika Jimbo la Tunduru Kusini inahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovolt 33 yenye urefu wa kilometa 9.4, ujenzi wa njia ya msongo wa umeme wa kilovolts 0.4 yenye urefu wa kilometa nane, ufungaji wa transfoma nne za KVA 50 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 275. Gharama za kupeleka umeme katika vijiji hivyo ni shilingi milioni 644.

Mheshimiwa Spoika, vijiji 57 vya Kata za Chiwana, Mchuluka, Mtina, Nalasi, Mchoteka, Ligoma, Tuwemacho na Lukumbulu vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya III, mzunguko wa pili unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021. ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO (K.n.y. MHE. ESTER A. BULAYA) aliuliza:-

TANESCO Mkoa wa Mara katika zoezi la kupeleka umeme vijijini walipitisha nguzo za umeme kwenye maeneo ya watu katika Kijiji cha Nyabeu, Kata ya Guta na uthamini ulifanyika na iliahidi malipo kufanyika lakini hadi leo hawajalipwa na badala yake wanaambiwa maeneo hayo ni ya TANESCO:-

(a) Je, ni lini Serikali itawalipa wananchi hao fidia stahiki?

(b) Je, ni kwa nini TANESCO inamiliki maeneo kabla ya kulipa fidia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Amos Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, miradi ya kupeleka umeme katika Wilaya za Serengeti, Bunda na Ukerewe ilitekelezwa kati ya mwaka 2003 na 2006 chini ya ufadhili za Serikali za Sweden na Hispania kupitia Mashirika yake ya Kimataifa ya Maendeleo SIDA na Spanish Funding Agency pamoja na Serikali ya Tanzania. Kazi ya tathmini ya mali za wananchi waliopisha mradi ilifanywa na Mtathmini Mkuu wa Serikali na malipo yalifanyika mwaka 2009. Ulipaji wa fidia hiyo ulifanyika kwa kuwashirikisha Watendaji wa Vijiji, Kata, Tarafa, Wilaya na Mkoa kuridhia orodha ya wananchi waliostahili kulipwa fidia hiyo. Jumla ya Sh.135,820,993 zililipwa kwa wananchi waliopisha mradi huo ikiwa ni pamoja na wananchi wa Kijiji cha Nyabeu.

Mheshimiwa Spika, TANESCO huchukua maeneo baada ya kufanya tathmini kupitia Mthamini Mkuu wa Serikali na kuwalipa wananchi wanaopisha ujenzi wa mradi.
MHE. MARY D. MURO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalipa fidia Wananchi wa Kiluvya, Madukani, Mwanalugali na Mikongeni ambao wamepisha ujenzi wa njia ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mbunge wa Viti Maalumu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inatekeleza mradi wa kujenga njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovot 400 kutoka Kinyerezi (Dar es Salaam) na Rufiji (Pwani) kupitia Chalinze hadi Dodoma kupitia maeneo ya Kiluvya, Madukani na Mwanalugali. Mradi huu unalenga kuongeza upatikanaji wa umeme katika ukanda wa Mashariki, Kati na Kaskazini mwa nchi kutoka katika mitambo ya kuzalisha umeme ya Kinyerezi na mradi wa Rufiji.

Mheshimiwa Spika, upimaji wa njia na uthamini wa mali za wananchi watakaopisha mradi ulikamilika mwaka 2018. Jumla ya shilingi bilioni 21 na milioni 600 zinatakiwa kulipwa kama fidia kwa wananchi katika maeneo ya Halmashauri za Kisarawe, Kibaha Mjini na Kibaha Vijijini ikiwemo wananchi wa Vijiji vya Chalinze, Kiluvya madukani na Mwanalugali. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 50 kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wananchi wa maeneo hayo baada ya kukamilisha uhakiki wa madai hayo.


Mheshimiwa Spika, Serikali inawaomba wananchi wavute subira wakati Serikali inaendelea kukamilisha taratibu za malipo haya, ahsante sana.
MHE. MARWA R. CHACHA (K.n.y. MHE. AGNESS M. MARWA) aliuliza:-

Nyumba nyingi za Vijijini hazikuwekewa umeme wakati wa usambazaji japo baada ya kuweka umeme kumekuwa na ongezeko la ujenzi wa nyumba na uzalishaji mali kama ujasiriamali.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha nyumba zote zilizobaki zinapata umeme kabla mradi wa REA haujamaliza muda wake?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Mathew Marwa Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, lengo la Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ni kupeleka umeme katika Vijiji vyote Tanzania Bara ifikapo Juni, 2021. Ili kutekeleza azma hiyo, Serikali imeweka kipaumbele kwa kusambaza miundombinu ya umeme katika maeneo ambayo hayajafikiwa na miundombinu ya umeme na katika Taasisi zinazotoa huduma za kijamiii kama vile Shule, Zahanati, Makanisa, Misikiti, Vituo vya Afya, Nyumba za Makazi na Biashara na Miradi ya Maji. Utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya III mzunguko wa kwanza ulianza kutekelezwa mwezi Julai, 2018 na unaendelea katika maeneo yote nchini ambapo utekelezaji wake utakamilika ifikapo mwezi Juni, 2019. Maeneo yatakayobaki ikiwa ni pamoja na nyumba za makazi, Taasisi, miradi ya maji na biashara yatapelekewa umeme kupitia mradi wa REA III Mzunguko wa pili utakaoanza kutekelezwa mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mpango huo, Serikali imebuni miradi ya ujazilizi (Densification) kwa lengo la kujaziliza katika mapungufu kwa miradi iliyotangulia. Miradi hii ya ujazilizi inalenga hasa kuhakikisha nyumba zote katika kila Kijiji na Kitongoji zinaendelea kupata umeme. Shirika la Umeme nchini (TANESCO) nalo linaendelea kusambaza na kuunganisha wateja mara kwa baada ya miradi ya REA kukamilika. Ili kuhakikisha wananchi wote wa Vijijini wanaunganishiwa umeme kwa gharama nafuu ya shilingi 27,000, ahsante sana.
MHE. ALLAN J. KIULA aliuliza:-

Serikali ya Awamu ya Tano inatekeleza mpango kabambe wa kusambaza umeme vijijini chini ya mpango wa REA:-

(a) Je, ni lini vijiji vyote 70 vya Wilaya ya Mkalama vitapata umeme wa REA II?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuweka umeme katika vitongoji vinavyopitiwa na njia ya umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Allan Joseph Kiula, Mbunge wa Iramba Mashariki, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza dhamira yake ya kufikisha umeme katika vijiji vyote nchini ifikapo mwezi Juni, 2021 vikiwemo vijiji 70 vya Wilaya ya Mkalama. Katika Awamu ya Pili ya utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme vijijini (REA II), jumla ya vijiji 14 vya Wilaya ya Mkalama viliwekwa katika mpango wa utekelezaji wa kupatiwa umeme kupitia Mkandarasi M/S JV EMEC & Dynamics.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwezi Aprili, 2019 vijiji vinne vya Nkito Kinyantungu, Nkito Nkurui, Ibaga Sekondari na Ibaga Centre viliwashwa umeme na wateja zaidi ya 100 wameunganishwa umeme. Kwa sasa, Mkandarasi anaendelea na kazi ya kuunganisha umeme katika vijiji 10 vilivyobaki ambapo kazi hiyo itakamilika ifikapo mwezi Juni, 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji na vitongoji vilivyopitiwa na miundombinu ya umeme katika Wilaya ya Mkalama vimejumuisha katika mpango wa kupatiwa umeme kupitia Mradi wa Ujazilizi (densification) awamu ya pili unaotarajia kuanza mwezi Julai, 2019. Aidha, mradi huo utahusisha pia kuvipatia umeme vitongoji vyote vya Wilaya ya Mkalama vilivyopitiwa na njia za umeme kupitia utekelezaji wa mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea. Mradi huu utakamilika mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. ALLY S. UNGANDO aliuliza:-

Wananchi wanaoishi katika Jimbo la Kibiti hutumia nishati ya mkaa na kuni kwa matumizi ya nyumbani, shuleni, gerezani na kadhalika, hivyo kusababibisha uharibifu mkubwa wamazingira kwa kukata miti hovyo:-

(i) Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka nishati mbadala?

(ii) Je, ni aina gani ya nishati itakayotumka badala ya kuni na mkaa?
NAIBU WAZIRI WA WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swal la Mheshimiwa Ally Seif Ungado, Mbunge wa Kibiti, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Sera ya Taifa ya Nishati ya mwaka 2015 (The National Energy Policy, 2015) imetoa mwongozo wakuboresha maisha ya wananchi kwa matumizi bora ya nishati kupitia teknolojia ya kisasa badala ya kuni na mkaa. Aidha, Serikali imekuwa ikichukua jitihada za makusudi kuendeleza vyanzo mbalimbali vya nishati ili kuongeza mchango wa nishati mbadala katika upatikanaji wa nishati nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha muda wa kati kuanzia mwaka 2015 hadi 2020, Serikali inatekeleza miradi ya kuzalisha umeme kupitia vyanzo vya gharama nafuu vya maji na gesi ikiwa ni mkakati ya kuwawezesha wananchi kumudu kutumia nishati vya umeme wa gharama nafuu kwa ajili ya kupika badala ya kuni na mkaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanza kutekeleza mradi wa kusambaza gesi asilia katika Miji ya Mtwara, LIndi, Pwani na Dar es Salaam ikiwa ni nishati mbadala ili kupunguza matumizi ya kuni na mkaa. Kwa kuwa sehemu ya kuni na mkaa unaotumika katika Jiji la Dar es Salaam huzalisha katika Wilaya ya Kibiti, hatua ya kuanza kutumia gesi asilia kwa kupikia itapunguza uharibifu mkubwa wa mazingira kupitia ukataji miti hovyo kwa matumizi ya kuni na mkaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua nyingine tarehe 18 Mei, 2018, Serikali kupitia Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) ilisaini kataba nakampuni ya Mihan Gas Limited kwa ajili ya kusambaza vifaa vya kupikia, mitungi ya gesi na majiko kwa kutumia liquidifies Petroleum Gas au gesi ya mitungi kwa watumishi wa umma na wananchi wengine. Mpango huo pia unalenga kupunguza matumizi ya mkaa na kuni.
MHE. CECIL D. MWAMBE (K.n.y. MHE. DAVID E. SILINDE) aliuliza:-

Zoezi la usambazaji wa umeme wa REA katika Wilaya ya Momba bado haujakamilika hadi sasa:-

(a) Je, ni lini Serikali itaanza mchakato wa kupeleka umeme katika kata ambazo hazijafikiwa na miradi hiyo katika Jimbo la Momba?

(b) Je, ni lini mradi wa kuwasha umeme Tarafa ya Kamsamba utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Momba ina jumla ya vijiji 72, kati ya hivyo, Vijiji 13 vya Nkangano, Chiwanda, Isanga, Kakozi, Ndalambo, Chitete, Tindingoma, Ntungwa, Mkonko, Kamsamba, Masanyinta, Itumbula na Mpapa, vimepata umeme kupitia Mradi wa REA II na wateja wa awali 854 wameunganishiwa umeme. Jumla ya Vijiji 15 vya Halmashauri ya Momba vya Nakawale, Ikana, Ivuna, Ipatikana, Muungano, Myunga, Machindo, Mfuto, Isanga, Tindingoma na Kikozi vimepatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza unaoendelea kutekelezwa na Kampuni ya STEG International Services. Kazi za kupeleka umeme katika vijiji hivi itakamilika ifikapo mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa kilometa 168 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 na kilometa 109 za njia za umeme msongo kilovoti 0.4, kufunga transfoma 37 na kuunganisha wateja wa awali 1,775. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 11.23. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2019, mkandarasi ameshafunga transfoma 15 kati ya 21 na kuwasha umeme. Jumla ya wateja wa awali 244 wameunganishiwa umeme. Mkandarasi anaendelea na kazi ya kuvuta waya kufunga transfoma katika Vijiji vya Ipata, Mpui, Msungwe na Kapele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tarafa ya Kamsamba ilipatiwa umeme kupitia Mradi wa REA awamu ya pili ambapo kazi ya kusambaza umeme katika baadhi ya vitongoji vya tarafa hiyo inaendelea chini ya TANESCO kwa bei ya shilingi 27,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kukamilika kwa Mradi wa REA awamu ya tatu, mzunguko wa kwanza, jumla ya vijiji 24 vitapatiwa umeme katika Halmashauri ya Momba. Vijiji 44 vilivyosalia vitapatiwa umeme katika Mradi wa REA II, mzunguko wa pili unaotarajia kuanza mwezi Julai, 2020.
MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza:-

Afya za wanawake wengi vijijini zinaathiriwa na moshi wa kuni wanazopikia kwenye majiko ya mafiga matatu ambayo yanatumia kuni nyingi na hivyo kuchochea kasi ya ukataji miti:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuondoa matumizi ya majiko ya mafiga matatu kote nchini?

(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka wa kuondoa majiko hayo kwenye shule zote za msingi na sekondari?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shally Josepha Raymond, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, matumizi ya tungamotaka hususan kuni na mkaa kama chanzo cha nishati ya kupikia hapa nchini yanakadiriwa kufikia asilimia 85. Matumizi ya tungamotaka ikiwemo mafiga matatu husababisha madhara ya kiafya kutokana na kuvuta hewa chafu inayotokana na kuni na mkaa kwa watumiaji pamoja na uharibifu wa mazingira kutokana na ukataji wa miti.

Mheshimiwa Spika, kupitia Sera ya Taifa ya Nishati ya mwaka 2015, Serikali imekuwa ikihamasisha matumizi bora ya nishati ikiwemo teknolojia zinazopunguza gesi ya ukaa na matumizi makubwa ya kuni na mkaa kwa kutumia majiko banifu. Aidha, Serikali imekuwa ikihamasisha kuacha matumizi ya nishati mbadala wa kuni na mkaa katika kupikia gesi na mitungi (Liquefied Petroleum Gas), bayogesi, vitofali vya mabaki ya tundamotaka na majiko ya nishati jua.

Mheshimiwa Spika, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini pamoja na jukumu la kusambaza umeme vijijini inasaidia usambazaji wa teknolojia bora za kupikia hususan katika taasisi za Umma nchi nzima zikiwemo Shule, Magereza, Kambi za Wakimbizi na Zahanati.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:-

Katika eneo linalopatikana gesi aina ya carbondioxide (CO2) kwenye Jimbo la Busekelo, Kijiji cha Mpata kuna visima ambavyo ni hatari kwa binadamu na viumbe hai wengine kwani huwa wanakufa wakivuta hewa ya sehemu hiyo:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kunusuru maisha ya binadamu na viumbe katika eneo hilo?
NAIBU WAZIRI NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fredy Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busekelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa katika Jimbo la Busekelo, katika Kijiji cha Mpata kuna visima vya gesi ya ukaa (Carbondioxide) vinavyomilikiwa na Kampuni ya Tanzania Oxygen Limited. Kampuni hiyo inamiliki leseni mbili za uchimbaji wa gesi ya ukaa ambazo ni ML 139/2002 iliyotolewa tarehe 17/11/2002 na ML 379/2009 iliyotolewa tarehe 21/08/2009. Kisima cha Mpata Kipo katika leseni Na. ML 139/2002.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la Mpata kuna visima viwili. Kisima kimoja kilichimbwa na kimefunikwa madhubuti na Kampuni ya Tanzania Oxygen Limited ambayo inavuna gesi ya ukaa. Kisima cha pili kimetokana na nguvu za asili zilizosababishwa na mlipuko wa volkano na hivyo kupelekea uwepo wa kisima cha asili. Kutokana na uwepo wa kisima hicho kilichotokana na njia ya asili, tafiti za awali zinatoa tahadhari ya kisima hicho kikifunikwa kinaweza kutoa gesi hiyo kupitia njia nyingine na hivyo kuleta madhara yasiyotarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maeneo hayo ili kudhibiti athari inayoweza kutokea. Hatua za udhibiti zilizochukuliwa na Serikali kwa kushirikiana na TOL ni pamoja na kuweka vizuizi madhubuti, uzio na ulinzi wakati wote kwa watu na wanyama ili wasiweze kufika katika eneo la kisima sambamba na kuweka mabango ya tahadhari katika eneo hilo. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na TOL inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu hatari za gesi ya ukaa katika maeneo yanayozalishwa gesi hiyo. Ahsante.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa Gridi ya Taifa Mkoani Katavi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri na Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dada yangu Anna Richard Lupembe Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) inatekeleza Miradi mbalimbali ya kusafirisha umeme itakayohakikisha kuwa Mikoa yote nchini inaunganishwa katika gridi ya Taifa ikiwemo Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa sasa kupitia shirika la umeme nchini (TANESCO) inatekeleza Mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Katavi kupitia Ipole na Inyonga yenye urefu wa kilomita 381 ili kuunganisha Mkoa wa Katavi katika gridi ya Taifa. Kazi hiyo pia itahusisha ujenzi wa vituo vya kupoza umeme wa msongo wa kilovoti 132/33 vya Ipole, Inyonga na Mpanda Mkoani Katavi. Gharama za mradi huu ni Shilingi bilioni 135.3.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tarehe 11 Oktoba, 2019 Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa mradi huu katika eneo la Orio Mjini Mpanda. Kazi zinazoendelea kwa sasa ni ujenzi wa vituo vya kupoza umeme vya Mpanda, Ipole na Inyonga pamoja na upimaji wa njia ya kusafirisha umeme kwa ajili ya tathmini ya mali za wananchi watakaopisha mradi. Kazi za ujenzi wa mradi huu zinatekelezwa kwa kutumia wataalam wa TANESCO kupitia kampuni tanzu ya ETDCO. Mradi huu unatarajiwa kukamilika kabla ya mwezi Mei, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia imeanza kutekeleza Mradi mkubwa wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 400, Iringa - Mbeya – Tunduma - Sumbawanga – Mpanda - Kigoma – Nyakanazi (North West Grid) yenye urefu wa kilomita 1,384. Mradi huu upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Shughuli za ujenzi wa mradi huu zitaanza mwezi Mei, 2020 na zinatarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha 2022/2023.
MHE. JOHN P. KADUTU aliuliza:-

Mradi wa Usambazaji Umeme Vijijini (REA) unaendelea kote nchini. Katika Jimbo la Ulyankulu bado umeme haujafika katika maeneo mengi:-

(a) Je, ni lini sasa umeme utasambazwa katika Kata za Uyowa, Silambo, Igombe Mkulu, Seleli, Nhwande na Kanoge?

(b) Hivi karibuni Wilaya ya Kaliua imesajili Shule za Sekondari tano (5) na Vituo vya Afya pamoja na Sekondari ya Mkondo; je, ni lini sasa umeme utafikishwa katika taasisi hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Peter Kadutu, Mbunge wa Ulyankulu, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi wa kufikisha umeme katika vijiji vyote nchini vikiwemo vijiji 49 vya Jimbo la Ulyankulu kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Kwanza unaoendelea. Jumla ya Vijiji 19 vinatarajiwa kupatiwa umeme ambavyo ni Mwongozo, Mapigano, Mwanduti, Kanoge, Utamtamke, Iyombo, Ikonongo, Mbeta, Kagera, Ulanga, Imara, Kanindo, Nhwande, Keza, Mkiligi, Ilege, Konane, Busondi na Seleli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 127.96; njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 76; ufungaji wa transfoma 38 za KVA 50 na KVA 100 pamoja na kuunganishia umeme wateja wa awali 1,246. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 6.8 na kwa sasa mkandarasi JV Pomy Octopus na Intercity anaendelea na kazi mbalimbali za miundombinu ya umeme katika kata 12 zikiwemo Kata za Kanoge, Nhwande, Seleli na Igombe Mkulu. Kazi za kufikisha umeme katika vijiji hivyo itakamilika ifikapo mwezi Juni, 2020.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Kwanza, taasisi zote za huduma za kijamii zikiwemo afya, elimu na maji zinapewa kipaumbele. Kwa sasa mkandarasi anaendelea na kazi ya kupeleka umeme katika Kituo cha Afya cha Mkondo na Shule ya Sekondari Mkondo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. NAGHENJWA L. KABOYOKA) aliuliza:-

Umeme wa maji unaonekana kuwa wa bei nafuu, na Same kuna maporomoko ya Mto Hingilili yanayoangukia Kata ya Maore na ya Mto Yongoma yanayoangukia Kata ya Ndungu; na Chuo cha Ufundi Arusha wameonesha utaalamu mkubwa wa kutengeneza umeme kwa kutumia maji hayo:-

Je, Serikali ipo tayari kukiwezesha Chuo hicho ili kiweze kujenga mitambo ya kuzalisha umeme wa maji Kata za Maore na Ndungu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua muhimu ya awali katika uendelezaji wa mradi wa kufua umeme ukiwemo wa maporomoko ya maji ni kufanya upembuzi yakinifu ambapo pamoja na mambo mengine tathmini ya wingi wa maji katika kipindi cha kuzalisha umeme (water resource assessment) lengo ni kujua kiasi cha umeme utakaozalishwa na gharama za kutekeleza mradi na manufaa yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Serikali kupitia TANESCO na wadau wengine inaendelea kufanya tathmini za awali katika vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme wa maporomoko ya maji makubwa na madogo ikiwemo maporomoko ya Mto Hingilili. Tathmini hizo zitafanyiwa kazi kulingana na matokeo yake na maeneo yanayohusika yatajulishwa ikiwa ni pamoja na Chuo cha Ufundi Arusha.
MHE. MARY P. CHATANDA aliuliza:-

Umeme umekuwa ukikatika mara kwa mara Korogwe na kufanya uharibifu wa mali za Wananchi:-

Je, ni lini tatizo hilo litapatiwa ufumbuzi.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mary Pius Chatanda, Mbunge wa Korogwe Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kutokana na ukarabati wa miundombinu ya umeme unaoendelea kwa sasa Wilayani Korogwe, TANESCO hulazimika kukata umeme katika maeneo husika ya wilayani humo ikiwa ni pamoja na maeneo ya Mji wa Korogwe. Hali hiyo inasababishwa na kazi zinazoendelea za kukarabati wa miundombinu ikiwa ni pamoja na kubadilisha vikombe vibovu, nguzo mbovu, ukataji wa miti na matawi katika njia za umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kazi za kukarabati miundombinu ya kusambaza umeme zifanyike hulazimika kuzima umeme katika maeneo yanayofanyiwa ukarabati. Kukamilika kwa ukarabati unaoendelea kutawezesha kuimarika kwa umeme na kurudi katika hali yake ya kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara zote kabla ya kuzima umeme taarifa zimekuwa zikitolewa katika vyombo mbalimbali vya habari katika Wilaya ya Korogwe na Mkoa wa Tanga. Hali ya kukatika umeme kwa ajili ya kupisha matengenezo kumeimarisha sana upatikanaji wa umeme katika maeneo hayo. Aidha, tunaomba wananchi waendelee kuwa wavumilivu katika kipindi cha matengenezo ya miundombinu hiyo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST (K.n.y. MHE. SAED A. KUBENEA) aliuliza:-

Gesi asilia iliyogundulika nchini ni takribani ujazo wa trilioni feet 56:-

(a) Je, uwekezaji wa viwanda vinavyotumia gesi asilia kwa ukanda wa Kusini umefikia wapi na ni wa kiwango gani?

(b) Je, mpango wa kujenga kiwanda cha kuchakata gesi asilia bado upo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saed Ahmed Kubenea, Mbunge wa Jimbo la Ubungo, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, gesi asilia iliyogundulika nchini hadi sasa ni futi za ujazo trilioni 57.54. Mikoa ya Lindi, Mtwara, Pwani na Dar es Salaam ni maeneo yaliyonufaika na shughuli za uwekezaji katika viwanda vinavyotumia gesi asilia. Matumizi ya gesi asilia nchini yalianza tangu mwaka 2004 ambapo kufikia mwezi Oktoba, 2019, jumla ya viwanda 48 vimeunganishwa na mtandao wa gesi asilia. Viwanda hivyo vinatumia gesi asilia kama nishati na vingine vinazalisha umeme kwa matumizi ya viwanda.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa mradi wa kusindika gesi asilia kuwa kimiminika (LNG) unaendelea. Kwa sasa utekelezaji wake umefikia hatua ya majadiliano ya mkataba wa nchi husika (Host Government Agreement) kati ya wawekezaji na Serikali. Ahsante.
MHE. ALMAS A. MAIGE Aliuliza:-

Mradi wa REA III(1) unatekelezwa katika Jimbo la Tabora Kaskazini kwa kasi ndogo na mpaka sasa ni vijiji vitatu tu kati ya vijiji 82 ndiyo vimewashwa umeme.

(a) Je, Serikali inachukua hatua gani kumfanya mkandarasi akamilishe kuwasha umeme katika vijiji vyote 18 vya REA III(1)?

(b) Kwa vile kwa makosa Mradi wa REA III(1) unarudiwa kupelekwa katika Kijiji cha Upuge, Kata ya Upuge ambako umeme ulishapelekwa na REA III. Je, ni lini sasa umeme utapelekwa katika Kata ya Ikongolo ambako ni Kata jirani na Kata ya Upuge?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Almasi Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi wa kufikisha umeme katika vijiji vyote nchini vikiwemo vijiji vya Jimbo la Tabora Kaskazini. Katika Jimbo la Tabora Kaskazini, Vijiji 18 vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III(1) unaoendelea kutekelezwa na Mkandarasi Kampuni ya JV Pomy Engineering Company Limited, Intercity Builders Limited na Octopus Engineering Limited. Ili kuhakikisha mkandarasi anakamilisha kazi za kuwasha umeme katika vijiji 18 vinavyofanyiwa kazi, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) pamoja na TANESCO wameimarisha usimamizi wa kazi za kila siku za mkandarasi na kumtaka mkandarasi kuwa na vifaa kwa ajili ye ujenzi wa mradi kutoka ndani ya nchi.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Kata ya Ikongolo vinavyojumuisha Kanyenye, Kiwembe na Majengo vitapelekewa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa REA III(2) utakaoanza mwezi Januari, 2020. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji vya kata hizo utahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovolt 33 yenye urefu wa kilometa 36.14, njia ya umeme wa msongo wa kilovolti 0.4 yenye urefu wa kilometa 20.28, ufunguaji wa transfoma tisa za KVA 50 na KVA 100 pamoja na kuwanungnishia umeme wateja wa awali 614 na gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 2.29.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY Aliuliza:-

Katika mradi wa REA I na II vijiji vingi vya Jimbo la Mbulu Mjini havikufikiwa na umeme na katika vijiji vilivyofikiwa ni kaya kati ya 20 mpaka 30 pekee ndizo zilizopata umeme:-

(a) Je, ni lini REA III itapeleka umeme katika Vijiji 26 vya Jimbo la Mbulu Mjini?

(b) Awamu ya I na II ziliruka shule nyingi, vituo vya afya na Makanisa. Je, ni lini sasa taasisi hizo zitapelekewa umeme?

(c) Je, ni lini Serikali itarudia usambazaji wa umeme katika vijiji vyote vilivyosambaziwa sehemu ndogo sana katika Jimbo la Mbulu Mjini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utekelezaji wa Mradi wa REA III, Mzunguko wa Kwanza katika Jimbo la Mbulu Mjini, jumla ya Vijiji vitatu vya Gwaami, Tsaayo na Banee vitapatiwa umeme na Mkandarasi Kampuni ya Angelique International Limited.

Aidha, vijiji vitatu vya Murray, Silaroda na Gunyoda vinaendelea kupelekewa umeme na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kwa Mpango wa Umeme Vijijini. Vijiji 20 vilivyobaki vya Jimbo la Mbulu Mjini vya Hereabi, Maheri, Kuta, Qwam, Nahasey, Hayasali, Hasama, Hayloto, Kwermusi, Amowa, Gwandumehhi, Aicho, Gedamar, Qalieda, Laghanda mur, Gidamba, Qatesh, Landa, Tsawa na Jaranja vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III, Mzunguko wa Pili unatarajiwa kuanza Januari, 2020.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, shule, vituo vya afya na taasisi nyingine ambazo hazijaunganishwa umeme katika vijiji au maeneo ya karibu yaliyounganishwa umeme na miradi ya awali ikiwemo REA I na II yatapelekewa umeme katika kipindi hiki. Tumetoa wito kwa Halmashauri au taasisi husika zilipie gharama za kuunganisha umeme ili taasisi hizo ziunganishiwe umeme.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maeneo ya Mbulu Mjini yaliyosambaziwa umeme, tunawaomba wananchi wa maeneo ya karibu na maeneo yenye umeme kuendelea kulipia Sh.27,000 ili maeneo hayo nayo yatumie umeme huo uliopo katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA (K.n.y. MHE. AZZA H. HAMAD) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itawapa huduma ya umeme wananchi wa Vijiji vya Buyubi, Itwangi, Imenya, Nyambui na Mwankanga ambao muda mrefu wamekuwa watazamaji wa nguzo za umeme unaokwenda maeneo mengine?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Azza Hillal Hamad, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi wa kufikisha umeme katika vijiji vyote nchini vikiwemo vijiji 126 vya Wilaya ya Shinyanga Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji 22 kati ya vijiji 126 katika Wilaya ya Shinyanga Vijijini vina umeme. Vijiji 50 vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA III, Mzunguko wa Kwanza unaotekelezwa na Mkandarasi Angelique International Limited ambapo hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Agosti, 2019 jumla ya vijiji 19 vimeshawashiwa umeme na ujenzi wa miundombinu unaendelea katika vijiji vilivyobaki na wateja zaidi ya 211 wameunganishiwa umeme. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi itakamilika ifikapo mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji 50 vya Wilaya ya Shinyanga Vijijini inahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 170.9; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 156; ufungaji wa transfoma 78 za KVA 50 na KVA 100 na kuunganisha umeme wateja wa awali 2,241. Gharama za mradi ni shilingi bilioni
10.7 na mradi unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji 54 vilivyobaki vikiwemo vijiji vya Buyubi, Itwangi, Imenya, Nyambui na Mwankanga vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III, Mzunguko wa Pili unaotarajia kuanza mwezi Januari, 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. SAED A. KUBENEA (K.n.y. MHE. JOHN J. MNYIKA) aliuliza:-

Bado tatizo la kupungua na kukatika kwa umeme bado linaendelea na baadhi ya maeneo hayajafikishiwa umeme mpaka sasa.

(a) Je, ni kwanini matatizo ya kukatika au kupungua kwa umeme katika Jimbo la Kibamba halijapatiwa ufumbuzi kinyume na Serikali ilivyoahidi?

(b) Je, ni maeneo gani katika Jimbo la Kibamba mpaka sasa TANESCO haijafikisha umeme na lini yatafikiwa?

(c) Je, kuna mkakati gani wa kupunguza gharama za wananchi kuunganisha umeme au kuwarejeshea wanapovuta wenyewe umbali mrefu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa John John Mnyika, Mbunge wa Kibamba lenye sehemu (a) (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la kukatika kwa umeme katika Jimbo la Kibamba linatokana na zoezi la kuhamisha miundombinu ya umeme ili kupisha upanuzi wa barabara ya Dar es Salaam - Morogoro. Kwa sasa tatizo hilo limepungua, baada ya zoezi hilo kukamilika kwa asilimia 97 na itakamilika mapema mwezi Juni, 2019. Hali ya upatikanji wa umeme katika Jimbo la Kibamba imeimalika kutokana na kukamilika kwa kazi ya kubadilisha nguzo mbovu na kukata miti kwenye mkuza wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 kutoka Ubungo hadi Kibamba. Vilevile kupitia TANESCO imetenga shilingi bilioni 5 kwenye bajeti ya 2018/19 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Mloganzila, Luguruni, chenye uwezo wa MVA 90, kituo hiki kitasambza umeme katika maeneo mbalimbali ya Jimbo la Kibamba, ikiwa ni pamoja na Hospitali ya Mloganzila na hivyo kutatua tatizo la ongezeko la mahitaji ya umeme katika Jimbo la Kibamba.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Kibamba kuna baadhi ya maeneo ya ambayo hayajapatiwa huduma ya umeme ikiwa ni pamoja na maeneo ya Kibesa, Kisopwa, Kipera, King’azi, Msumi na baadhi ya maeneo ya Mpigi na Kwembe. Katika bajeti ya mwaka TANESCO ilienga shilingi bilioni 3.78 kwa ajili ya kupeleka umeme katika maeneo ya Kwembe kwa Tendwa, Kwembe Kipera, Mbezi Luis, Kibwegere, Msakuzi, Mpigi CCM ya Zamani, Kibamba Delini, Mpiji, Kwembe, Msumi na King’azi. Kazi ya kupeleka umeme katika maeneo haya inaendelea na itakamilika mwezi Septemba, 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yaliyosalia ya Kibesa, Kisopwa na Kipera, yatapatiwa umeme kupitia bajeti ya 2019/20.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Mwezi Desemba, 2013, Serikali kupitia EWURA ilipunguza gharama za kuunganisha umeme kutoka shilingi 385,682, hadi 272,000 kwa wateja wa njia moja wa mjini, aliye ndani ya mita 30 ikiwa ni punguzo la asilimia 30. Kanuni za Sheria ya Umeme Kifungu 131 ya mwaka 2008 zilizotangazwa katika gazeti la Serikali Na. 63 la Tarehe 4 Februari, 2011 zinaelekeza TANESCO na mteja kukubaliana namna ya kurejeshwa kwa gharama zilizotumika kujenga miundombinu ya umeme kama TANESCO haitakuwa na uwezo wa kibajeti kwa wakati huo kumfikishia mteja huduma ya umeme.
MHE. DKT. TULIA ACKSON (K.n.y. MHE. SAUL H. AMON) aliuliza:-

Umeme wa REA umepita katika vijiji vya Unyamwanga, Kisonidzela na Mpuga lakini wananchi wa maeneo hayo hawajaunganishiwa huduma ya umeme.

Je, ni lini wananchi hao wataunganishiwa huduma ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saul Henry Amon Mbunge wa Rungwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe ni miongoni mwa halmashauri zilizonufaika na utekelezaji wa mradi wa REA II uliotekelezwa na mkandarasi kampuni ya SINOTEC Ltd. kutoka nchini China ambapo vijiji vya Unyamwanga na Kisonidzela ni miongini mwa vijiji vilivyopatiwa huduma ya umeme.

Mheshimiwa Spika, kupitia utekelezaji wa mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea kutekelezwa na Mkandarasi STEG International Services jumla ya vijiji 26 katika Wilaya ya Rungwe vitafikishiwa umeme ikiwemo kijiji cha Mpuga.

Mheshimiwa Spika, kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa kilomita 20 za njia ya umeme wa msongo kilovoti 33, kilomita 42 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 25 na kuunganisha wateja wa awali 1,195. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 2.25

Mheshimiwa Spika, baadhi ya vitongoji ambavyo havikufikiwa na umeme katika utekelezaji wa REA II katika vijiji vya Unyamwanga na Kisonidzela vitapatiwa umeme kupitia mradi wa ujazilizi Awamu ya II Densification II utakaoanza na kutekelezwa kuanzia mwezi Julai, 2019 ahsante sana.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE (K.n.y. MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA III katika Kata za Bujula, Nyamalimbe, Kamena, Nyalwanzaka, Nyakamwaga, Busanda Kaseme, Magenge, Butindwe na Nyaruyeye?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la mhesimiwa Lolesia Jeremiah Bukwimba, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inapeleka umeme katika Jimbo la Busanda kupitia Mradi wa REA III Mzunguko wa Kwanza ambapo Kata ya Nyaruyeye itapatiwa umeme kupitia Mkandarasi Kampuni ya JV White City International Contractors. Na kazi ya kupeleka umeme katika Kata ya Nyaruyeye itakamilika mwishoni mwa Mwezi Mei, 2019 ambayo ni wiki hii.

Mheshimiwa Spika, katika Kata nyingine za Nyalwanzaja, Kamena, Busanda na Nyakamwaga zitapata umeme kupitia utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme katika vijiji vinavyopitiwa na mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa Gridi ya Taifa ya Msongo wa Kilovoti 220 kutoka Bulyanhulu hadi Geita. Hadi mwezi Mei, 2019 mkandarasi amekamilisha kazi za kufanya survey na kazi za ujenzi wa mradi zinatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Januari, 2021. Katika Kata zilizobaki za Magenge, Nyamalimbe, Bujula na Kaseme zitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA III Mzunguko wa Pili unaotarajiwa kuanza Mwezi Julai, 2019.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA III katika Kijiji cha Hemsambia na Vitongoji vyake vyote?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula, Mbunge wa Mkinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Hemsambia na Kindundui ni miongoni mwa Vijiji vya Kata ya Kigongoi, Wilaya ya Mkinga vilivyofaidika na Awamu ya Tatu ya utekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini, REA III, mzunguko wa kwanza. Mkandarasi Kampuni ya Ubia ya JV Radi Service Limited, Njarita Contractor Limited na Aguila Contractor Limited yuko site anaendelea na kazi ya kusambaza umeme katika maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, kazi za kupeleka umeme katika Vijiji vya hemsambia na Kindundui imejumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 2.1, njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa mbili, ufungaji wa transfoma mbili za KVA 50 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 62. Gharama ya mradi ni shilingi milioni 184.23.

Mheshimiwa Spika, vijiji vingine vya Kata ya Kigongoi vya Vuga, Kwekuyu, Kindundui, Mgambo Shashui na Bombo Mbuyuni vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA III Mzunguko wa Kwanza unaoendelea kutekelezwa Wilayani Mkinga na kukamilika mwezi Juni, 2020. Ahsante sana.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-

Serikali aliahidi kupeleka umeme katika vijiji vyote vya Jimbo la Mbulu Vijijini kupitia REA III kwa sababu REA II haikufanya vizuri katika jimbo hilo:-

Je, vijiji vingapi vitafikiwa na umeme wa REA Awamu ya III?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay Mbunge wa Mbulu Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imedhamiria kufikisha umeme katika vijiji vyote visivyo umeme nchini ifikapo Juni 2021. Jimbo la Mbulu Vijijini lina vijiji vipatavyo 76 na kati ya vijiji hivyo 12 vimepatiwa umeme. Vijiji 13 vya Qaloda, Getesh, Endesh, Labay, Maretadu, Hayderer, Endanachan(Haydom), Muslur, Dirim, Simha, Yaeda Ampa, Endoji na Gidhim vimejumuishwa katika mradi wa REA III mzunguko wa kwanza. Mkandarasi Kampuni ya Angelique International Limited kutoka India anaendelea na kazi za kusambaza umeme katika Jimbo la Mbulu Vijijini. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji vilivyopelekewa umeme zitakamilika mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi zinazoendelea kwa sasa ni pamoja na kusimika nguzo, kuvuta nyaya na kufunga transfoma katika Vijiji vya Qaloda, Getesh, Endoji, Endesh, Labay, Maghang Juu, Getagujo na Simahha. Kati ya vijiji hivyo, vijiji 6 vya Getesh, Endoji, Qaloda, Labay, Getagujo na Maghang Juu vitawasha umeme mwisho wa mwezi Mei, 2019. Kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa kilometa 45.87 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 na kilometa 35 za njia ya umeme wa msongo kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 16 na uunganishaji wa wateja wa awali 347 na gharama za mradi ni shilingi bilioni 2.6.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vilivyobaki katika Jimbo la Mbulu vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa pili utakaoanzwa kutekelezwa mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-

Vijiji vya Sintali, Nkana, Nkomachindo na Katani viko kwenye mpango wa kupata umeme wa REA Awamu ya III lakini mpaka sasa hakuna kazi zinazoendelea:-

Je, ni lini kazi hiyo itaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata Mbunge wa Nkasi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya vijiji 51 vitapatiwa umeme katika Wilaya ya Nkasi ikiwa ni pamoja na vijiji 12 vya Jimbo la Nkasi Kusini vya Ntuchi, Tambaruka, Chima, Chatelekesha, Isasa, Kingombe, Ntemba, Nkomolo II, Kasapa, Kisula, Namansi na Kasu B. hadi kufikia mwezi Mei, 2019 umeme tayari umeshawasha katika vijiji vya Chala, Chima, Chala Isasa na Ntemba. Jumla ya wateja wa awali 77 wameunganishiwa umeme. Aidha, mkandarasi anaendelea na kazi katika vijiji 9 viliovyosalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za mradi katika Jimbo la Nkasi Kusini vinahusisha ujenzi wa kilometa 29.65 za njia ya umeme wa msongo kilovoti 33; kilometa 28 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4; ufungaji wa transfoma 14 na uunganishwaji wa wateja wa awali 324. Gharama za kazi hiyo inakadiriwa kufikia shilingi bilioni 2.15.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vya Sintali, Nkana, Katani na Nkomachind vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa pili unatarijiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA (K.n.y. MHE. CATHERINE V. MAGIGE) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha mchakato wa ulipwaji fidia kwa wananchi zaidi ya 2,000 wa Wilaya ya Longido na Monduli ambao maeneo yao yalipitiwa na Mradi wa Umeme Vijijini (REA)?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Valentine Magige, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini inatekeleza mradi wa kupelea umeme katika vijiji vyote nchini ifikapo mwezi Juni, 2021. Lengo la mpango huu ni kuhakikisha kuwa Watanzania zaidi ya asilimia 85 wanatumia umeme ifikapo mwaka 2025. Ili kuhakikisha lengo hili linafikiwa, Serikali inagharamia miundombinu, ujenzi na gharama ya kufikisha huduma hii ya umeme kwa wananchi kwa asilimia 100 na wananchi kulipa shilingi 27,000 tu ikiwa ni Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ya huduma hiyo. Hivyo, miradi ya umeme vijijini haina fidia.

Mheshimiwa Spika, naomba kutumia fursa hii kuwaomba wananchi wa Longido, Monduli na Watanzania wengine kutoa ushirikiano katika utekelezaji mradi huu ikiwa ni pamoja na kutodai fidia, nakushukuru.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Jimbo la Singida Kaskazini limepata Mradi wa Umeme Vijiji (REA na BTIP) ambapo utapeleka umeme katika vijiji 54 kati ya 84; katika baadhi ya maeneo ambayo mradi umepita umeacha nyumba za wananchi, taasisi za dini, taasisi za Serikali na pampu za maji pasipo kuziunganishia umeme.

(a) Je, Serikali ina kauli gani kwa maeneo hayo yaliyorukwa na wananchi waliokwishafanya wiring kwa matarajio ya kuunanishiwa umeme?

(b) Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji 30 vilivyosalia?

(c) Je, Serikali ipo tayari kusaidia njia mbadala ya umeme wa jua (solar power) katika maeneo ya huduma muhimu kama zahanati, sekondari na huduma za maji wakati tukisubiri usambazaji katika vijiji vilivyosalia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishaji Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme vijijini kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Lengo la mradi huu ni kuhakikisha umeme katika vijiji, taasisi, viwanda na miradi ya maji na maeneo yaliorukwa katika Jimbo la Singida Kaskazini zikiwemo nyumba za wananchi, taasisi za dini, taasisi za Serikali na pampu za maji zitapelekewa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea na kupitia Mradi wa Densification II utakaoanza kutekelezwa mwezi Juni, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2020.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza miradi ya kusambaza umeme vijijini ambapo vijiji 30 vilivyosalia katika Jimbo hilo vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa mradi wa REA III utakaoanza kutekelezwa kuanzia mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.

(c) Mheshimiwa Spika, mwaka 2018/2019 Serikali kupitia Mradi wa Results Based Finance unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) iliendelea kufanya utafiti ya kujua kiasi cha nguvu ya jua kinachopatikana nchini ikiwa ni pamoja na eneo la Singida Kaskazini.

Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika kwa utafiti huo Serikali itaanza kazi ya kupeleka miundombinu ya umeme wa nguvu za jua katika Jimbo la Singida Kaskazini. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Katika Jimbo la Korogwe Vijijini bado vijiji vingi havina umeme.

Je, ni lini usambazaji wa umeme kupitia REA utakamilika katika vijiji vya Jimbo la Korogwe Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kutekeleza mradi wa kupeleka umeme katika vijiji vyote nchini hadi ifikapo mwezi Juni, 2021. Katika Jimbo la Korogwe Vijijini jumla ya vijiji 71 vitaunganishiwa umeme. Aidha, vijiji 14 vya Hamashauri ya Wilaya ya Korogwe Vijijini vinatarajiwa kupatiwa umeme kupitia Mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea kutekelezwa. Hadi kufikia mwezi Juni, 2019 Mkandarasi Kampuni ya DERM Electrics ameshawasha umeme katika vijiji vinne vya Nkalekwa, Magila, Kwasunga na Welei pamoja na kuunganisha umeme kwa wateja wa awali zaidi ya 112.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa mkandarsi anaendelea na kazi ya kusimika nguzo, kuvuta nyaya na kufunga transifoma katika vijiji kumi vitakavyopatiwa umeme kupitia mradiwa REA lll mzunguko wa kwanza. Kazi za mradi katika Jimbo la Korogwe Vijijini zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 9.45, njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 48 na ufungaji wa transfoma 18 za kVA 50 na 100, pamoja na kuunganisha umeme kwa wateja wa awali 825 na gharama za mradi ni shilingi bilioni moja na milioni 600.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vilivyosalia 57 vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa pili, unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. JULIUS K. LAIZER aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA kama ilivyoahidi katika vijiji vya Munjere, Baraka, Mbaasha, Lepurko, Mti Mmoja, Arkatan, Arkaria, Mfereji, Ndonyonaado, Mswakini, Naitolia, Emurua, Lashaine, Orkenswa, Engaaroji, Oldonyolengai na Naalarami?

(b) Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Shule ya Sekondari Oldonyolengai ambayo laini imefika tangu mwaka 2015 lakini mpaka sasa umeme haujawaka?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Julias Kalanga Laizer, Mbunge wa Monduli lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imedhamiria kufikisha ueme katika vijiji vyote visivyo na umeme nchini ifikapo mwezi Juni 2021. Kulingana na mpango wa kupeleka umeme katika vijiji 64 Wilayani Monduli vijiji 16 vilishapatiwa umeme vikiwemo vijiji vya Arkatani na Mti Mmoja ni miongoni mwa vijiji vya Wilaya ya Monduli vilivyopata umeme kupitia awamu ya pili ya mradi wa kusambaza umeme Vijijini (REA II). Aidha, vijiji vya Arkaria, Lepurko na Mbaasha vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea.

Mheshimiwa Spika, kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 48.75 na njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 40 na ufungaji wa transfoma 20. Jumla ya wateja wa awali 720 wataunganishiwa umeme na gharama za mradi ni shilingi bilioni tatu. Mradi unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2020.

Vijiji vingine vya Munjere, Baraka Mfereji, Ndonyonaado, Mswakini, Naitolia, Emurua, Lashaine, Orkenswa, Engaaroji na Naalarami vitapata umeme kupitia REA III mzunguko wa pili utakaoanza kutekelezwa kuanzia mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.

(b) Mheshimiwa Spika, Shule ya Sekondari Oldonyolengai iliyopo Kata ya Engaruka imeshapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea kutekelezwa Wilayani Monduli.
MHE. ALLY S. UNGANDO aliuliza:-

Jimbo la Kibiti lina Kata 5 na Vijiji 17, sawa na Vitongoji 72 ambavyo vipo kwenye maeneo ya Delta lakini havina umeme:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka umeme kwenye Visiwa hivyo?

(b) Je, utapelekwa umeme wa aina gani?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Seif Ungando, Mbunge wa Kibiti lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia umuhimu wa kuwapatia huduma wananchi wake Serikali kupitia TANESCO ilifanya upembezi yakinifu kwa ajili ya kupeleka umeme katika vijiji vya Pombwe, Kiongoroni, Mbuchi, Mbwera Mashariki, Mbwera Magharibi, Maporoni, Kiechuru, Msala, Kiasi, Kiomboni, Mchinga na Mfisini vilivyo katika Delta ya Mto Rufiji. Aidha, katika hatua hiyo imesaidia kupata mahitaji halisi na kubaini changamoto zilizopo katika kutekeleza mradi wa kufikisha umeme katika vijiji hivyo. Mradi wa kupeleka umeme katika maeneo hayo tajwa unatarajiwa kutekelezwa kuanzia mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Desemba, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya upembuzi yakinifu kufanyika vijiji vya Mbuchi, Mbwera Mashariki na Mbwera Magharibi vitaunganishiwa na umeme wa Gridi ya Taifa kutoka Muhoro umbali wa kilomita 40. Ujenzi wa njia ya umeme itatumia nguzo za zege kwa kuwa maeneo mengi ni chepechepe na oevu. Vijiji vingine vilivyobaki vitapelekewa umeme wa solar kwa kuwa ujenzi wa laini ya umeme wa Gridi kupeleka katika vijiji hivyo umekuwa na changamoto kutokana na jiografia ya maeneo hayo, ahsante.
MHE. DEVOTHA M. MINJA (K.n.y. MHE. SUSAN L. KIWANGA) aliuliza:-

Kata za Mchombe, Igima, Mbingu, Namwawala na Idete katika Jimbo la Mlimba zilipelekewa mradi wa umeme kwa gharama nafuu lakini mradi huo umefanywa vibaya na hivyo kusababisha wananchi wengi kukosa umeme:-

(a) Je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwa wananchi hao?

(b) REA ilikabidhiwa mkandarasi kupima maeneo yatakayounganishwa umeme katika vijiji vya Msolwa, Miembeni, Iduimdembo, Ipungusa, Matema, Lumumwe, Uchindile, Kitete na Ngwasi katika Awamu ya Pili; Je, kwa nini kazi hiyo inasuasua?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa umeme kwa gharama nafuu (Low Cost Design) katika Mkoa wa Morogoro ulitekelezwa katika vijiji 14 vya Wilaya ya Kilombero. Kazi za mradi zilihusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 35.2; njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 82.6; ufungaji wa transfoma 262 za KVA 15 na 25; pamoja na kuunganisha umeme wateja 4,671. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 6.935.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwezi Desemba, 2018 vijiji vyote 14 vya Mkusi, Njage, Ngajengwa, Igima, Mbingu, Kisegese, Namawala, Idete Magereza, Miwangani, Katurukira, Mihelule, Mikoleko, Msolwa Station na Nyange vilipatiwa umeme na wateja 4,286 waliunganishwa na huduma ya umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mradi huo wa Low Cost Design katika Wilya ya Kilombero hususan Jimbo la Mlimba, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Awamu ya Tatu Mzunguko wa Kwanza inapeleka umeme katika Jimbo la Mlimba katika vijiji vya Ipugusa, Msolwa, Kalengakelu, Miembeni, Iduindembo, Ipungusa, Matema, Lumumwe, Uchindile, Kitete, Idandu na Ngwasi. Kazi zinazofanywa kwa sasa ni pamoja na kusimika nguzo, kuvuta nyaya na kufunga transfoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia utekelezaji wa mradi huu, Kijiji cha Kalengakelu kimepatiwa umeme na wateja zaidi ya 20 kutoka Vitongoji vya Usalama na Samora vimeunganishiwa umeme. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi itakamilika mwezi Juni, 2020, ahsante sana.
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA aliuliza:-

Kasi ya utekelezaji wa miradi ya REA III Jimboni Bagamoro ni ndogo:-

Je, ni lini miradi hiyo itakamilishwa katika Jimbo la Bagamoyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Shukuru Jumanne Kawambwa, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea na utekelezaji wa usambazaji wa umeme katika Mkoa wa Pwani ambapo Bagamoyo ni miongoni mwa wilaya zinazonufaika na mradi unaoendelea kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya vijiji 10 vya Jimbo la Bagamoyo vimejumuishwa katika utekelezaji wa mradi wa REA III, mzunguko wa kwanza unaoendelea. Hadi kufikia tarehe 25 Juni, 2019, vijiji vyote 10 ambavyo ni Kongo, Kimarang’ombe, Kitopeni, Kiharaka (Kiembeni na Minazi Minane), Matimbwa (Ugongomoni na Kibahengwa), Udindivu KKKT, Fukayosi, Kimele A&B, Mto wa Nyanza na Migude vimepatiwa umeme na wateja wa awali 927 wameunganishiwa umeme. Kazi inayoendelea kwa sasa ni kuunganisha wateja katika vijiji vyote vilivyotajwa kadri wanavyolipia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivyo imejumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 9.84; njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 37.14; ufungaji wa transfoma 21 za KVA 50 na 100 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,154. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 2.05. Kazi ya kusambaza umeme katika mradi huu utakamilika ifikapo mwezi Juni 2020.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Vijiji vya Mpepai na Lipilipili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Raphael Mapunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi wa kusambaza umeme vijijini katika vijiji vyote vya Tanzania Bara. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2021. Mradi wa REA III unaoendelea utapeleka umeme katika vijiji 50 vya Wilaya ya Mbinga kupitia Mkandarasi Namis Corporate Ltd anayetekeleza kazi hiyo katika Mkoa wa Ruvuma.

Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Mpepai na Lipilipili pamoja na vijiji vingine vilivyobaki katika Wilaya ya Mbinga vitapatiwa umeme kupitia Mradi unaoendelea. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji vya Mpepai na Lipilipili inahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 18, ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 22, ufungaji wa transfoma nane za KVA 50, 100 na 200, pamoja na kuwaunganishia huduma ya umeme wateja wa awali 313. Gharama ya mradi ni shilingi milioni 977.