Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Rose Cyprian Tweve (3 total)

MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu ni imani ya watanzania kuwa elimu bora ndiyo utakuwa msingi wa kuhakikisha vijana wa Taifa hili pale wanapohitimu wanakuwa na uwezo aidha wa kuajiriwa au kutumia knowledge na skills ambazo wamezipata shuleni kuweza kutambua fursa zilizopo ili waweze kujiajiri wenyewe. Sasa ni matumaini yangu Mheshimiwa Waziri Mkuu utakubaliana na mimi kuwa walimu bora ndiyo wenye uwezo wa ku-transfer au kuambukiza maarifa yaliyo bora kwa vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa swali langu kwako Mheshimiwa Waziri Mkuu, nilitaka kujua mkakati wa Serikali kuhakikisha tunatumia vijana ambao wana division one na two ili wawe walimu ambao tunategemea wata-train wanafunzi ambao watakuwa competent either kutumika kwenye nchi yetu au waweze kutoka nje ya nchi kujitafutia fursa kwa ajili ya maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tweve, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba vijana wetu wakipata elimu bora wanaweza kuingia kwenye Sekta ya Ajira, ajira binafsi hata zile rasmi nje na ndani ya nchi. Na hii inatokana na uimara wa utoaji elimu tulionao nchini ambao pia tunaendelea kuuboresha kila siku ili tuweze kufikia hatua hiyo ya kuwawezesha kuona fursa na kuweza kuzitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utaratibu ambao tumeuweka Serikalini ni kubainisha kati ya Wizara ya Elimu na TAMISEMI kwa usimamizi imara kwenye maeneo haya. Wizara ya Elimu kama msimamizi wa sera, yeye ndiye mwenye uwezo na ndiyo tumempa dhamana ya kuhakikisha kwamba tunaandaa walimu bora wenye uwezo kwa madaraja uliyoyataja na vigezo vinavyotumika kupeleka walimu ni vile ambavyo vimeshafafanuliwa. Tunao walimu wa shule za msingi, walimu wa sekondari lakini pia tuna walimu wa vyuo, maeneo yote yana sifa zake na wote hawa wanakwenda kama sifa zao zinavyoeleza.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, matokeo tunayoyapata sasa ni matokeo mazuri ya mipango ya Sera tuliyonayo lakini usimamizi wa utoaji elimu tumeipeleka TAMISEMI, wao ndiyo wanamiliki shule za msingi na sekondari kama elimu ya msingi kujihakikishia kwamba vijana wanaoandaliwa kwenda mpaka elimu ya juu ni vijana ambao walishapewa msingi imara wa kielimu. Kwa hiyo, kazi hii inaendelea kwa kuwa na walimu imara, bora lakini pia kuimarisha miundombinu na wote Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote ni mashahidi, tumepeleka fedha ya kutosha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, nyumba za walimu, maabara na vyumba vingine pamoja na vifaa mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mikakati hii yote inasababisha kuwa na elimu bora nchini na unapotoa elimu bora, unatoa matokeo yaliyo bora na vijana wanaopata matokeo hayo, sasa wanaweza kuziona fursa zao na kuweza kuzitumia. Kwa hiyo, mkakati wa Serikali unaendelea na tutaendelea kupokea ushauri wenu kuona naona nzuri ya kuboresha Sekta ya Elimu ili tuweze kufikia hatua nzuri, ahsante. (Makofi)
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kila mwaka Serikali imekuwa ikiongeza bajeti ya kupeleka kwenye Vyuo Vikuu ili watoto wasiokuwa na uwezo waweze kupata mkopo na kujikimu na mahitaji yao ya chuo. Utakubaliana na mimi kama Taifa tuna uhitaji mkubwa sana wa Watanzania hasa vijana wenye ujuzi hasa ujuzi wa kati ili sasa twende kuboresha na kupanua huduma muhimu kama vile afya, elimu, nishati na miundombinu vijijini. Sasa changamoto kubwa ya hawa vijana ambao tunawahitaji ambao wako kwenye vyuo vya kati hawana access ya hii mikopo na wao hawana uwezo wa kujilipia ada hizi.

Mheshimiwa Spika, sasa nataka kujua mkakati wa Serikali wa kuhakikisha hawa vijana ambao tunawahitaji ambao wako kwenye vyuo vya kati wanakuwa na access ya kupata hii mikopo kama ambavyo tunafanya vijana wa elimu ya juu? Nakushukuru sana. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tweve, Mbunge wa Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, anachosema Mheshimiwa Mbunge ni sahihi kwamba tuna kada ya elimu ya kati hawajaingia kwenye mkopo kama ambavyo mkopo huu unaendelea. Hii inatokana na sheria tuliyoiweka na ndiyo kwa sababu Bodi inaitwa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Sheria iliyoanzisha Bodi hii ilianza kwa kuelekeza elimu ya juu na ndiyo ambayo sasa tunayo. Toka tulipoanza mpaka sasa tumegundua kwamba mahitaji ni mapana mno, lakini upana huu wa mahitaji utategemea pia na uwezo wa kifedha wa Serikali. Tukiwa tunaendelea kuwanufaisha Watanzania kupitia elimu ya juu kwa vyuo tu vya elimu ya juu, bado tuna mafanikio lakini tuna changamoto zake, tunaendelea nazo. Tumegundua tuna uhitaji pia wa elimu ya kati ambayo ni kada ambayo inafanya kazi kubwa sana kwenye sekta mbalimbali mpaka viwandani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kadiri tunavyokwenda Serikali tutaleta Muswada ndani ya Bunge kama pia uwezo wa kifedha nao ukiwa mzuri na tutashiriki pamoja kujadili uwezekano wake ili kufungua mlango kwa vijana wa kada ya kati wa elimu ya kati ili na wao waweze kunufaika na mikopo hii. Kwa hiyo kadri tutakavyokuwa tunapata fedha, tutakuwa tunaendelea kuboresha kupanua wigo, tukifika elimu ya kati tutashuka mpaka elimu ya juu ya kawaida huku chini kwa maana ya sekondari kadiri tutavyopata fedha. Hiyo tutaileta Bungeni, tutajadili Waheshimiwa Wabunge na Mheshimiwa Tweve najua utakuwepo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri Mkuu ugonjwa wa malaria unasababisha vifo vya Watanzania wengi hususan wanawake wajawazito na watoto. Naishukuru Serikali iliona tatizo na wakaamua kufanya investment kubwa pale Kibaha, takriban Bilioni 46 kujenga kiwanda cha viuadudu na ikasaini mkataba na NDC kwa makubaliano kuwa watanunua zile dawa na kusambaza katika maeneo yote nchini ili tuweze kutokomeza ugonjwa huu lakini haijafanya hivyo.

Kutokana na takwimu kutoka Mpango wa Kudhibiti Malaria Nchini tunatumia takribani Bilioni 108 kwa mwaka kufanya warsha na matamasha mbalimbali na preventive measures kama net kupambana na ugonjwa huo.

Mheshimiwa Spika, sasa swali langu kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu nataka kujua mkakati wa Serikali kuhakikisha tunasaini mkataba tena na NDC wa kununua na kuhakikisha tunasambaza dawa hizi nchini kuhakikisha tunatokomeza janga hili ambalo linapoteza maisha ya Watanzania wengi. Nakushukuru sana. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tweve, Mbunge wa Mkoa wa Iringa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali yetu imefanya uwekezaji mkubwa sana pale Kibaha Mkoani Pwani, kwa kujenga kiwanda kikubwa sana kinachotengeneza viuadudu na ili kurahisisha masoko, Wizara ya Afya pamoja na Ofisi ya Rais - TAMISEMI, zimeingia mkataba wa kununua viuadudu na kuvisambaza kwenye hospitali zetu, Vituo vya Afya na hospital za Wilaya, Zahanati pia maeneo kama shule na taasisi zote ambazo zinakusanya vijana wengi na kuna tatizo la mbu. Kama sehemu ya awali ya soko mbali ya soko ambalo tunauza pia nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, utaratibu huu tuliingia mikataba ya kwamba kiwanda kile moja kati ya mteja atakuwa ni Serikali yenyewe kupitia Wizara zote mbili ili kukabiliana na tatizo la malaria inayosababishwa na mbu. Ni kweli kwamba Serikali inasimamia mauzo ya dawa hizo ndani na nje ya nchi, ziko Halmashauri ambazo bado hazijatekeleza wajibu wake wa kwenda kuchukua viuadudu, lakini baadhi ya hospitali ambazo ziko chini ya Halmashauri hazijapata huduma hiyo kupitia Halmashauri hizo. Mpango wa Serikali katika hili ni kuhakikisha kwamba tunawasisitiza Wakurugenzi wa Halmashauri kununua viuadudu vile ili wapulize kwenye maeneo ya makazi ya wananchi kupunguza kiasi cha mbu ili kupunguza ugonjwa wa malaria. Kwa hiyo, nachukua wazo lako na swali lako kama ushauri kwa Serikali tuimarishe mikataba, tupitie mikataba ili tuweze kusambaza dawa ile itusaidie: -

(i) Itapunguza tatizo la malaria inayosababishwa na mbu;

(ii) Tunaimarisha soko ambalo tunaliendesha kupitia uwekezaji mkubwa wa fedha ambazo umezitamka Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, hivyo, naomba nitoe wito kupitia swali hili kwa Halmashauri zote nchini lakini na hospitali za Mikoa zilizo chini ya Wizara ya Afya, kuhakikisha kwamba tunanunua viuadudu vinavyozalishwa kwenye kiwanda chetu ambacho Serikali na yenyewe ina hisa ili tuweze kupuliza kwenye makazi ya watu, maeneo ya jumuiya, tuweze kuua mazalia umbu na tuwe salama ugonjwa wa malaria ambao unasabishwa na mbu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo utaratibu na mkakati wa Serikali kwenye eneo hili. Ahsante sana. (Makofi)