Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Munde Abdallah Tambwe (3 total)

MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuuliza swali kwa Waziri Mkuu. Kwa kuwa Serikali ina mifumo, sheria, miongozo na taratibu ya upelekaji wa fedha za maendeleo katika Halmashauri zetu mara tu baada ya bajeti ya Serikali kwisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kuwa sheria hizi na miongozo hii haifuatwi na kupelekea Halmashauri zetu kupelekewa robo tu ya fedha au nusu tu ya fedha zikiwemo Halmashauri zangu za Mkoa wa Tabora ambazo zote saba hazijawahi kupata fedha kamili. Hii inaleta taharuki kubwa ndani ya Halmashauri zetu. Je, Mheshimiwa Waziri Mkuu unatoa kauli gani kuhusu ucheleweshwaji wa fedha za bajeti kwenda kwenye Halmashauri zetu kwa wakati muafaka?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabla sijaanza kujibu swali, uridhie kuwakumbusha Watanzania kwamba leo hii Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anatimiza siku ya 365 kwa maana ya mwaka mmoja. Naamini Watanzania wote tumeona utendaji wake na hasa mwelekeo wake wa kuiongoza Serikali hii kwa mafanikio. Jukumu letu ni kumwombea Mheshimiwa Rais aweze kuendelea vizuri na kuiongoza nchi yetu na wananchi wote tuungane pamoja kila mmoja kwa dhehebu lake kuiombea Serikali hii iweze kupata mafanikio makubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nianze kujibu swali la Mheshimiwa Munde kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali yetu baada ya bajeti inawajibika kutekeleza maamuzi ya Bunge letu hasa katika kupeleka fedha za bajeti zilizopangwa. Hata hivyo, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote mnajua kwamba baada ya Bunge kuridhia na kutoa mamlaka ya matumizi ya fedha, Serikali hii tulianza na majukumu muhimu; moja, ilikuwa kwanza kujiridhisha kuwepo kwa mifumo sahihi ya makusanyo ya mapato na matumizi yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, mbili kwa upya wake tulianza kupeleka watumishi watakaosimamia shughuli za usimamizi wa ukusanyaji wa mapato na matumizi yake kwenye Halmashauri zote nchini. Kazi kubwa ya tatu ilikuwa ni kuratibu na kutathmini miradi yote iliyokuwa imeanza halafu ilikuwa haijaendelezwa na ile miradi mipya ili tuweze kutambua pamoja na thamani zake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuwa tumejiridhisha sasa tumeanza kupeleka fedha kwenye Halmashauri zote nchini. Kwa mujibu wa kumbukumbu kutoka Hazina ambazo wakati wote tunapewa taarifa; ofisini kwangu pia napewa taarifa; kufikia mwezi Oktoba tumeshapeleka zaidi ya shilingi bilioni 177 za miradi ya maendeleo kwenye Halmashauri zetu nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge watabaini wiki hizi tatu tumeanza kuona kwenye magazeti yetu mengi matangazo mengi ya zabuni kutoka kwenye Halmashauri mbalimbali. Hii ina maana kwamba tayari miradi ile ambayo ilikuwepo na ile ambayo inaendelea na mipya imeshaanza kutengewa fedha na kuanza kutangazwa kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo. Kwa hiyo, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba sasa Serikali itaendelea na upelekaji wa fedha kwenye Halmashauri kwa ajili ya shughuli zetu za maendeleo kwenye Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, bado msisitizo umebaki pale pale kwamba Halmashauri ziendelee kukusanya mapato ya ndani ili kuongezea bajeti kwa fedha za Serikali ambazo tunazipeleka na tumesisitiza ukusanyaji huo uwe ni wa mfumo wa kielektroniki ili kudhibiti mapato ambayo tunayapata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, tumeendelea kusisitiza matumizi sahihi ya fedha ambazo tunazipeleka kwenye Halmashauri kwamba fedha hizi ni lazima zitumike kadiri ilivyokusudiwa kwa miradi iliyoandaliwa kwenye Halmashauri zenyewe.
Waheshimiwa Wabunge, sisi wenyewe ni Wajumbe wa Baraza letu la Madiwani kwenye Halmashauri zetu; niendelee kuwasihi kusimamia na kufuatilia matumizi ya fedha tunazopeleka kwenye Halmashauri ili ziweze kutekeleza miradi ile kikamilifu. Serikali itaendelea kutuma fedha kwenye Halmashauri zetu kadri miradi ile ilivyoweza kuratibiwa. Ahsante.
MHE. MUNDE A. TAMBWE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuuliza swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu umekuwa mfuatiliaji mzuri wa mazao ya wakulima huko mikoani ili waweze kupata tija. Umekuja Tabora mara kadhaa, umetoa maelekezo kadhaa kuhusu suala zima na kero za tumbaku, lakini agizo kubwa ulilolitoa la kuhakikisha tumbaku iliyopo ndani ya wakulima na kwenye magodauni ya msimu uliopita inunuliwe, ambayo mpaka leo hii ninavyoongea tumbaku hiyo bado haijanunuliwa. Hii imesababisha adha kubwa kwa wakulima wa tumbaku wa Mkoa wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ni msimu wa kulima tumbaku nyingine lakini tumbaku iliyopo ni ya mwaka wa jana na haijanunuliwa; na tumbaku hii ikikaa kwa muda mrefu inashuka grade ambapo ubora wa tumbaku unapungua na inateremka uzito. Mpaka sasa ma-godown mengi yanavuja na tumbaku hiyo kuvujiwa na kusababisha hasara kubwa na tahaluki kubwa kwa wakulima wa tumbaku Mkoa wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Tabora wana imani kubwa na Serikali ya Awamu ya Tano na leo wanakuomba sana, wanakusihi wapo chini ya miguu yako wameniagiza; wanaomba utoe tamko.

Je, Serikali inatoa tamko gani leo kuhusu kununua tumbaku ya msimu uliopita ambayo bado haijanunuliwa, iliyopo kwenye magodauni ya wakulima wa Mkoa wa Tabora?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Munde, Mbunge wa Tabora kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la zao la tumbaku ni jambo ambalo Serikali tumelifanyia kazi kweli kweli, na zao la tumbaku ni miongoni mwa mazao ambayo tunataka sasa yapate mabadiliko ya kilimo chake, lakini pia na masoko yake. Moja kati ya tatizo ambalo lipo sasa ni lile aliloeleza mheshimiwa Mbunge la masoko ya tumbaku na Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote wanaotoka kwenye maeneo ya tumbaku wanajua jitihada za Serikali zilizofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la tumbaku upo utamaduni wa kila mwaka wa wakulima wetu na makampuni yanayonunua kufunga mikataba ya kiwango cha tumbaku kitakachonunuliwa na makampuni na ndicho kiwango ambacho wakulima wanapaswa kulima.

Mheshimiwa Spika, jambo lililojitokeza mwaka huu ni kwamba wakulima wamelima zaidi ya kiwango kilichowekewa mikataba ya kununuliwa kwenye msimu. Kwa hiyo, tumbaku ambayo imebaki sasa ni ile ya ziada ya msimu ya bajeti ambayo makampuni yanayonunua yalitaka yanunue tumbaku. Ile tumbaku yote ambayo ilikuwa kwenye bajeti ilishanunuliwa, hii ni ile ya ziada.

Mheshimiwa Spika, Serikali ziada hii hatujaiacha kama ambavyo tunaona sasa, ni kwamba makampuni yenyewe tumekaa nayo, tumeyasihi yaweze kununua tumbaku. Wameeleza kwamba walikuwa nje ya bajeti na walikuwa wanaendelea kuzungumza na vyanzo vyao vya fedha ili waje kununua tumbaku yote iliyobaki. Mjadala huo umeendelea na sasa upo mjadala wa bei kwa kuwa sasa imekuwa ni ziada ya mahitaji yao wao wanalazimisha na wanataka wanunue kwa kiwango cha chini, lakini Serikali tunataka wanunue angalau kwa bei dira ya zao lile.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo bado tumeendelea na jitihada za kutafuta nchi mbalimbali zinazoweza kununua tumbaku. Tumeenda Indonesia, China, Misri na Iran na nchi zote hizi zimeonyesha nia ya kuinunua tumbaku iliyopo sasa kwenye maghala yetu. Nchi ya Indonesia imefikia hatua nzuri, wanajadili kiwango cha tumbaku watakachochukua na sasa wanajadili kwenye eneo la bei. Watakapokamilisha mjadala wa kujua kiwango gani watanunua, Serikali sasa itaridhia.

Interest yetu Serikali ni kuona kwamba mwananchi ananufaika kwa kuuza tumbaku yake kwa bei nzuri ili sasa kila mkulima aweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nawasihi sasa Waheshimiwa Wabunge wenzangu, lakini pia wakulima wote wa zao la tumbaku, jana nimeona pia kwenye TBC tumbaku ipo pale Kaliua, nimemwona Mwenyekiti wa Halmashauri akieleza madhara yanayojitokeza kama ambavyo umeeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka tu nieleze kwamba jitihada za kilimo zitakapokamilika tutawapa taarifa ya hatua nzuri tuliyoifikia na hatua nzuri kwetu ni kutaka kununua tu hiyo tumbaku iliyobaki. Kwa hiyo, tunaendelea na bei tutawapa taarifa.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuuliza swali kwa Waziri Mkuu. Mheshimiwa Waziri Mkuu Tanzania ni nchi ambayo inaendelea kwa kasi kubwa katika uchumi wa viwanda hususan Serikali ya Rais Joseph John Pombe Magufuli; ambayo imejikita sana kwenye uchumi wa viwanda mpaka ambapo muda huu tunaviwanda zaidi ya 3,700; si jambo dogo. Lakini maendeleo haya ya kasi kubwa ya uchumi yanabidi yaendane na maendeleo ya wananchi. Je Mheshimiwa Waziri Mkuu mnamkakati gani kama Serikali kuhakikisha maendeleo ya kasi kubwa ya uchumi wa viwanda na kuhakikisha maendeleo ya watu vinakwenda sambamba?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Munde Mbunge wa Mkoa wa Tabora kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali yetu inayoongozwa na Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli imeelekeza kuboresha uchumi wake kupitia viwanda pia. Viwanda hivi baada ya kufanya study ya kuweza kuwafikia Watanzania na kuwapatia maendeleo; tunajua mchango wa viwanda popote palipo na kiwanda lazima kitumie mali ghafi na malighafi hizi ziko kwenye sekta ya kilimo, mifugo, uvuvi, maliasili pia hata madini. Kwa hiyo panapokuwa na kiwanda kinachohitaji malighafi hiyo obvious malighafi hiyo na wale wote wanaozalisha malighafi hiyo watakuwa wameboreshewa uchumi wao kwasababu tayari wanauhakika wa soko pale kwenye kiwanda. Ule uhakika wa soko tayari tunapeleka tunaunganisha manufaa ya uwepo wa kiwanda na hali na maisha ya wananchi wanaopata huduma hiyo kwenye kiwanda hicho.

Lakini viwanda hivi navyo vinavyofaida nyingine nyingi ambazo pia tunaunganisha na maendeleo ya mtu mmoja mmoja. Leo mgogoro wetu wa kukosekana kwa ajira, Rais weru alikuwa na muono wa mbali sana. Viwanda hivi sasa vinaajiri Watanzania kwenye maeneo kilimo; na wote mnajua kwamba hata kwenye ajira tumeweka tumebana kidogo mianya ya watu wengi kutoka nje kuajiriwa badala yake tumefungua milango kuajiriwa kwa Watanzania wenyewe. Kwahiyo viwanda vingi vinaajiri Watanzania kwahiyo angalau tumepunguza mgogoro wa kutokuwepo kwa ajira.

Lakini mbili kwa uwepo wa viwanda hivi tunapata kodi, kodi hizi ndizo ambazo zinatuwezesha leo kujenga zahanati, kujenga shule, kujenga miundombinu ya barabara na maeneo mengine. Kwahiyo tunaufanya uchumi wa viwanda tunaupeleka pia kwa jamii. Hatujaishia hapo tu viwanda hivi sasa vinazalisha malighafi ambazo leo tunakuwa na uhakika nazo kwa uzalishaji wake na ubora wake, lakini pia kwa gharama nafuu na upatikanaji wa karibu kuliko kuagiza vitu kutoka nje zaidi. Kwahiyo tumetengeneza uwepo wa soko la ndani la uhakika ambako sasa uchumi huu tunaupeleka sasa kwa wananchi. Kwahiyo kufungamanisha kwa viwanda na uchumi wa mtu mmoja mmoja hasa kumejikita kwenye maeneo hayo, namna ambavyo viwanda vinaleta tija kwa uwepo wake na kwa wananchi walioko jirani na kwa Tanzania nzima. Tunaendelea kuhamasisha ujenzi wa viwanda ili watanzania waweze kunufaika na uwepo wa viwanda hivyo.

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie Watanzania, tunaendelea kuhamasisha na kuita wawekezaji kutoka nje na ndani ya nchi tuendelee kuwekeza kwenye viwanda ili tuboreshe pia uzalishaji na kupata masoko wa malighafi inayotakiwa viwandani. Ahsante sana. (Makofi)