Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Martha Moses Mlata (2 total)

MHE. RITTA E. KABATI (K.n.y. MHE. MARTHA M. MLATA) aliuliza:-

Je, ni kwa nini Sherehe za Muungano zimekuwa zikifanyika na kupewa nafasi kubwa Kitaifa tu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Moses Mlata, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Singida, kama ifuatavyo-

Mheshimiwa Spika, Sherehe za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar huazimishwa kwa kuzingatia Mwongozo wa Maadhimisho na Sherehe za Kitaifa wa mwaka 2011 uliotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo ndiyo ina dhamana ya kuratibu sherehe zote za Kitaifa. Aidha, katika Mwongozo huo, Sura ya Tano katika maelezo ya Utangulizi imeelezwa kuwa “Sherehe za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar zitafanyika tarehe 26 Aprili ya kila mwaka katika uwanja wa Uhuru, Dar es Salam mahali ambapo udongo wa Tanganyika na Zanzibar ulichanganywa. Sherehe hizo zinaweza kufanyika nje ya Dar es Salam kama Kamati ya Maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa itakavyoelekeza”

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuzingatia Mwongozo huo wa Maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa hadi hapo kutakapokuwa na sababu za msingi zitakazofanya Mwongozo huo kufanyiwa marekebisho kwa nia ya kuuboresha. Hata hivyo, Serikali inahimiza wananchi kuadhimisha sherehe hizo kwa kufanya shughuli mbalmbali za maendeleo ikiwemo usafi, michezo, makongamano na shughuli mbalimbali za kijamii.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA (K.n.y. MHE. MARTHA M. MLATA) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga vizuri barabara za Kibaya - Urughu, Urughu – Mtekente na Mtekente – Ndago zilizopo Wilayani Iramba ili kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi wa eneo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Moses Mlata, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara za Kibaya – Urughu, Urughu – Mtekente – Kisonga na Mtoa – Kisonga – Ndago yenye urefu wa kilometa 61.46 zimekuwa zikifanyiwa matengenezo kwa nyakati tofauti ili kuhakikisha zinapitika nyakati zote.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 barabara ya Kibaya – Urughu ilifanyiwa matengenezo ya sehemu korofi kwa urefu wa kilometa 16 kwa gharama ya shilingi milioni 40.8 na pia barabara ya Mtoa – Kisonga – Ndago ilifanyiwa matengenezo ya muda maalum kwa urefu wa kilometa sita na makalvati matatu yalijengwa. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 barabara ya Urughu – Mtekente – Kisonga ilifanyiwa matengenezo ya sehemu korofi kwa urefu wa kilometa 12.5 kwa gharama ya shilingi milioni 53.3.

Mheshimiwa Spika, vilevile katika mwaka wa fedha 2018/2019, jumla ya shilingi milioni 188.8 zimetengwa kwa ajili ya kujenga box culvert kubwa la midomo miwili katika Mto Mtekente, kazi ya ujenzi imeanza na inatarajiwa kukamilika mwezi Agosti, 2019. Aidha, katika mwaka wa fedha 2019/2020 kupitia TARURA barabara ya Urughu – Mtekente – Kisonga imetengewa kiasi cha shilingi milioni 224.3 kwa ajili ya ujenzi wa box culvert kubwa katika Mto Kisonga na barabara ya Mtoa – Kisonga – Ndago imetengewa kiasi cha shilingi milioni 18 kwa ajili ujenzi wa kufanyiwa matengenezo ya sehemu korofi kwa urefu wa kilometa sita.