Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Martha Moses Mlata (1 total)

MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, ahsante; na mimi nashukuru kupata nafasi ili nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa, tarehe 15/05/2017 Serikali ilitangaza rasmi kuivunja Mamlaka ya Ustawishaji wa Makao Makuu Dodoma na majukumu yake kuhamishiwa Manispaa ya Dodoma, kwa hilo naipongeza Serikali. (Makofi)

Lakini kwa kuwa baadhi ya wananchi hata Waheshimiwa Wabunge pia walikuwa tayari wameshalipia viwanja na walikuwa hawajakabidhiwa. Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusu jambo hili? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Mlata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Rais alitoa agizo la kuvunja Mamlaka ya CDA na mamlaka hiyo na majukumu yake kuyahamishia Ofisi ya Rais – TAMISEMI, kupitia Manispaa ya Dodoma. Kazi hiyo imeshafanywa na zoezi linaloendelea sasa kwanza wale watumishi wote wa CDA watahamishiwa Manispaa ya Dodoma, lakini tutafanya mchujo kidogo, wale ambao walikuwa na malalamiko, wanalalamikiwa na wananchi wale wote tutawaweka pembeni, kwa sababu tunataka tupate timu mpya ambayo inafanya kazi vizuri.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbili, tunaendelea sasa na uhakiki na ukaguzi wa kina kwenye masuala ya fedha na utumishi wenyewe ili tuweze kuanza vizuri, tujue CDA ilipoacha iliacha na fedha kiasi gani na shughuli zake zilifikia hatua gani halafu pia kuweza kuendelea, lakini majukumu yote yanabaki kama yalivyokuwa na CDA yataendelea kufanywa na Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma. Kinachobadilika pale ni maandishi, kama kwenye risiti zilikuwa zinasomeka CDA, sasa zitasomeka Manispaa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilisha utaratibu huu mpango kazi wote utaendelea kama ulivyokuwa. Kama kuna mtu alilipa nusu anataka kumalizia, wataendela kukamilisha malipo yao, kama kuna mtu alishakamiliha hajapata kiwanja, ataenda kukabidhiwa kiwanja chake na namna yoyote ya utendaji wa kawaida utaendelea. Sasa hivi akaunti zote zimefungwa kwa hiyo, huwezi kulipa mpaka hapo tutakapofungua malipo.

Mheshimiwa Spika, tutamuagiza Mkurugenzi sasa wa Manispaa, atoe maelezo sahihi kwa Wana Dodoma na kwa Wananchi, Waheshimiwa Wabunge mkiwemo ili kila mmoja aweze kujua, lakini kwa kauli hii ndio usahihi wa taarifa ya CDA kwa namna ambavyo tumeivunja na tumehamishia Mamlaka pale Manispaa ya Dodoma na watumishi wote sasa watawajibika kwa Mkurugenzi wa Manispaa na hakutakuwa na chombo kingine pale.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ambayo tumewaelekeza sasa pale CDA kwenye Idara ya rdhi, kwenye lile jengo lisomeke Idara ya Ardhi - CDA na huko ndani tume- plan sasa Wizara ya Ardhi ipeleke mtu anayeandika Hati. Tunataka pale ndani iwe One Stop Centre. Ukienda kuomba ardhi, ukishapimiwa, ukishalipia, hati unapata humo humo kwenye hilo jengo. Kwa hiyo, tunataka turahisishe upatikanaji wa hati na viwanja kwenye jengo hilohilo moja, ukiingia ndani ukitoka unatoka na hati yako badala tena kwenda mahali pengine. Ahsante.