Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Martha Moses Mlata (26 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
shukrani kwa utaratibu huu mzuri ambao unatuwezesha kutoa mchango wetu kwa wale ambao hatujapata nafasi ya kuongea.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Waziri na Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara hii kubwa na ambayo ndiyo uti wa mgongo wa maendeleo na ukuzaji uchumi kwa Taifa letu hasa kwa wananchi walio wengi. Wizara hii ndiyo pekee itakayomwondolea umaskini mkulima, mvuvi na mfugaji pamoja na wote wanaotegemea mazao yatokanayo na sekta hizi. Naomba nitoe maoni yangu kama ifuatavyo:-
(i) Ukitaka mali utaipata shambani:-
(a) Endapo Waziri utawapatia nyenzo za kisasa wakulima wako kama trekta, power tiller, jembe la ng‟ombe na kadhalika;
(b) Mbolea, pembejeo za aina zote ambazo zitamfikia mkulima kwa wakati na za kutosheleza; na
(c) Maafisa Kilimo wapelekwe vijijini kuliko na wakulima ili watoe ushauri wa kitaalam.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ushauri huo, naomba Mkoa wa Singida uingizwe kwenye orodha ya mikoa inayolima mahindi kama zao la biashara ili kuweza kuwapatia pembejeo (mbegu) ya zao hili. Zao la vitunguu katika Mkoa wa Singida lipewe kiapumbele kama ni zao la biashara, pia na kupewa pembejeo. Zao la alizeti, bado wakulima wengi wanalima kwa mkono, hivyo, tunaomba trekta angalau kila Kijiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kuhusu matrekta ya SUMA JKT ambayo yalisaidia sana na ndiyo yaliyoinua ongezeko la kilimo kwa mazao yote, kwani yalikuwa yanatolewa kwa mkopo wa Halmashauri zilikuwa zinawadhamini wakulima na utaratibu huo uliwasaidia sana. Je, ni kwa nini SUMA JKT hawana tena utaratibu huo ambapo walishirikiana na TIB au Benki ya Kilimo?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishie hapo. Ombi langu ni:-
(i) Pembejeo ya zao la mahindi Singida;
(ii) Zana za kisasa za kilimo;
(iii) SUMA JKT warejeshe utaratibu wao wa kukopesha matrekta kwa kushirikiana na TIB kupitia Wizara ya Kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niaze kwa kutoa shukrani za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa zawadi kubwa ambayo ameitoa kwa wanasanaa wote kwa kitendo chake cha kutambua sekta hii na pia Wizara hakika tunampogenza kwa hili. Ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuitambua sekta ya sanaa na kuipa Wizara Mheshimiwa Rais ameweza kupatia katika uteuzi wake kwa kumteua Mheshimiwa Nape Moses Nnauye kuwa Waziri katika Wizara hii, kwani tuna imani kubwa na Mheshimiwa Nape pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Anastazia Wambura. Tunaamini ataifikisha mbali sekta hii, suala la msingi ni kwamba Wizara hii ipewe support hasa kwenye suala la bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo tayari wameshaanza kuifanya. Pia naomba nimpongeze Waziri kwa kuzindua Tamasha la Filamu la Kimataifa la Tanzanite tarehe 23 Aprili, pale Mount Meru Hotel, Arusha. Tamasha hili lina tija sana kwa Serikali na wadau wa sanaa, kutangaza kazi zao, kimataifa. Pia litatoa ajira kubwa kwa Watanzania, litaongeza idadi kubwa ya watalii kuja Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine naomba Mashirikisho ya Sanaa yaimarishwe ili yaweze kusaidia Wizara namna ya kuisaidia sekta hii. Mashirikisho hayo ni:-
(a) Filamu; waigizaji, waandishi wa miswada, uigizaji, wazalishaji na wasambazaji.
(b) Muziki; Muziki wa Dansi – CHAMUDATA, Muziki wa Injili - CHAMVITA, bongo flava, taarabu na rumba.
(c) Sanaa za Ufundi; tingatiga, uchoraji, ususi na ufinyanzi.
(d) Maonesho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini Wizara yako inayo orodha ya vyama vyote ambavyo ni wanachama katika mashirikisho yote kupitia BASATA. Hakika Mheshimiwa Waziri utakapotumia mashirikisho haya kuyawekea mkazo na utaratibu mzuri ni wazi utakuwa umeleta mafanikio makubwa sana. Kuna vyama ambavyo vimeshapiga hatua kubwa sana mfano, Chama cha Muziki wa Injili, kina matawi hadi mikoani japo si yote lakini chama kwa kupitia viongozi wake wamehamasisha na watu wengi (wasanii wa nyimbo/muziki wa injili) wamejiunga rasmi na kuna vitambulisho maalum.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni wameweza kujiunga na bima ya afya na wanachama wengi wameweza kupatiwa kadi za bima ya afya na hivyo kunaondoa adha kubwa ya wasanii wanapougua kuanza kuomba misaada wa kuchangiwa kwa ajili ya kulipia gharama za matibabu. Ninaamini utaratibu huu utaendelezwa kwa vyama vingine vilivyo wanachama wa mashirikisho husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, usambazaji wa kazi za sanaa bado ni tatizo kubwa, Waziri tunaomba uingilie kati jambo hili na hasa kwenye mikataba, kwani ndipo penye uonevu na wizi mkubwa wa haki ya msanii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria ya adhabu ya mtu anayekamatwa na uharamia wa kazi za sanaa bado inamlinda mhalifu kwa kupewa adhabu ndogo, nayo iangaliwe upya ili kukomesha wizi wa kazi za wasanii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, COSOTA itoe maelezo ya malipo ya mirahaba kwani ni muda mrefu sasa hawalipwi. Je, ni chombo gani sasa kitapewa kazi ya kusimamia takwimu na ukusanyaji wa fedha hizi na kujiridhisa kuwa ni kiasi gani zimekusanywa na zimeenda kwa nani na je, ndicho anachostahili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, CD na DVD (mazagazaga) zinazouzwa mitaani kwa bei ya shilingi 1000, kwanza Serikali inapoteza mapato kwa sababu hazina stamp za TRA hazijalipiwa kodi. Pia zinawaumiza wasanii wetu wa ndani ambao wamepitia mlolongo mrefu sana hadi kupata stamp za TRA. Pia naomba stamp hizi ziwekwe utaratibu wa kupatikana mikoa yote. Naomba niishie hapa na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na pongezi kwa Waziri, Mkuu wa Majeshi na Wakuu wa Vitengo vyote. Kazi ni nzuri na hakika tuna amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maombi, kulikuwa na mpango wa kujengwa kambi ya JKT Mkoa wa Singida, Wilaya ya Iramba Ndago, je, suala hili liliishia wapi? SUMAJKT walifanya vizuri sana kwenye suala la matrekta japo changamoto za uelewa wa waliochukua mkopo haukuwa wazi lakini kwa sasa limeshaeleweka. Hivyo, naomba warejeshe zoezi hilo la kuuza matrekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nakushukuru kwa nafasi hii. Kwa sababu bajeti hii inagusa na Mfuko wako wa Jimbo wa Bunge nilikuwa naanza nataka nianze kwa kutoa shukurani kwanza kwako, nikianza na Mwenyezi Mungu kwa hali hii niliyosimama hapa.

Mheshimiwa Spika, nina mwaka sasa zaidi na miezi kama mitatu/minne sijasimama hapa Bungeni kuchangia, lakini leo Mungu ni mwema sana kwangu, nimeweza kupata nafasi hii ya kuweza na mimi kusimama na kuongea mbele ya Bunge lako Tukufu kuweza kutoa mchango wangu. Mungu wetu ni mwema na atukuzwe sana, tuzidi kumwamini na kumtegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kumshukuru Mheshimiwa Rais, nikushukuru wewe kwa sababu Mfuko huu wa Bunge umetajwa na umetaja huduma za afya kwa Waheshimiwa Wabunge kwa ajili ya matibabu. Siwezi kusimama nianze kuzungumza tu bila kuupongeza mfuko huu ukiongozwa na wewe pamoja na Katibu wa Bunge na Viongozi wengine ukisaidiwa na Mheshimiwa Jenista Mhagama anayeshughulikia masuala ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, mmenitunza, mmenitibu na leo nimesimama hapa. Mungu akubariki sana na wote waliohusika. Naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye alifuatilia sana afya yangu. Mungu akubariki sana. Sina maneno mengine ya kusema, bali Mungu aendelee kukubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema maneno hayo, ninashukuru madaktari wote na Mheshimiwa Waziri Ummy pamoja na Naibu wake. Nasema waendelee hivyo kwa sababu wataokoa maisha ya watu walio wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya shukurani hizo, kwa kweli bado nitaendelea kutoa pongezi. Mheshimiwa Waziri Mkuu nakupongeza sana pamoja na Mheshimiwa Jenista Mhagama, tunaye Mheshimiwa Angellah Kairuki, tunaye Mheshimiwa Stella Ikupa mama yangu. Nikimtaja Mheshimiwa Stella Ikupa mama yangu, ninataka nimpongeze Mheshimiwa Rais, kwa sababu nami nikimtaja Mheshimiwa Stella Ikupa, mama yangu ni kama Mheshimiwa Stella Ikupa. Nafikiri mnanielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kutambua mchango mkubwa wa watu wenye ulemavu, kuwapa nafasi kubwa kwenye Serikali yake. Ameonesha kwamba anaweza. Ni kweli wanaweza. Mheshimiwa Rais Mungu ambariki sana, kwa sababu sisi ni watoto wa akina Mheshimiwa Mama Stella Ikupa kama Stella. Mama yangu amenilea mpaka nimefikia hapa nipo ndani ya Bunge, siyo kwa sababu ya ulemavu, bali ni kwa sababu wanaweza. Nakupongeza sana Mheshimiwa Stella Ikupa.

Mheshimiwa Spika, pia kijana wetu Mheshimiwa Mavunde, ni kweli vijana wanaweza na ameonesha mfano mzuri na vijana wataendelea kuaminiwa kwenye Uongozi Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyoifanya, nataka niseme ameongoza vizuri. Mawaziri wote tumewaona jinsi ambavyo wamechapa kazi kwa sababu yeye amekuwa mchapakazi. Nilikuwa namwita Mheshimiwa Mzee Kamwele pale, nimesema leo nitaanza kukuita mzee. Nilimwona ameingia kijana, lakini sasa hivi naona amezeeka; ni kwa sababu ya kuchapa kazi; asubuhi huku, jioni huku, usiku yumo, kwa hiyo, ni lazima anaonekana mzee kwa sababu amechapa kazi. Mheshimiwa Waziri Mkuu umeongoza kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, nikimwangalia Mheshimiwa Mzee Mpango pale, namwita Mzee Mpango kwa sababu aliingia kijana, sasa namwona ni mzee kwa sababu ya gwaride ambalo wamelichapa. Kwa kweli wanaweza, wamefanya kazi nzuri sana, ninaamini huko Majimboni watakapokwenda hawatakuwa na Wapinzani kabisa kwa sababu Taifa hili bado linawahitaji sana. Ni pongezi hizo za kwako Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo moja ambalo pia nataka tu nipongeze wakati namwangalia Mheshimiwa Mpango pale, kweli Watanzania wamelipa kodi sana. Mara ya kwanza tulikuwa tuna wasiwasi, watu wakasema kuna watu wanaondolewa leseni zao, miradi inafungwa, nani atakayelipa kodi? Kwa kweli tuna kila sababu ya kuwapigia makofi Watanzania, wamelipa kodi ndiyo maana maendeleo yamerudi kwao. Huu ni usimamizi mzuri wa Serikali, wamekuwa waadilifu walipa kodi na sisi tumerudisha.

Mheshimiwa Spika, ukirudi nyuma pesa ambazo tulikuwa tukipitisha hapa zilikuwa haziendi au zinaenda kidogo, lakini safari hii zimekwenda, watu wamefanya kazi. Michango imelipwa, kodi zimelipwa, maendeleo yamekwenda, ukienda kwenye upande wa afya, tumefanya vizuri; ukienda kwenye upande wa barabara, tumefanya vizuri; ukienda kwenye upande wa elimu, mpaka hii elimu bure, nilikuwa namwangalia yule mtoto wa pale Simiyu, machozi yalinitoka. Nikasema hivi isingekuwa elimu bure, mtoto genius kama huyu tungemwona wapi? Sasa kwa sababu ya elimu bure, kuna watoto wengi kama yeye ambao hatukuwaona wameweza kufanya vizuri na wamebadilisha maisha yao. Kwa kweli nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na tunampongeza Mheshimiwa Rais, hongera sana.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa afya ukienda hata kule kwetu Mkalama kwa Wahadzabe tulikuwa hatuna hospitali, lakini sasa hivi aka! Mambo ni safi. Akina mama wakiingia, mtoto wake wa kike, wa kiume anatoka salama bila matatizo, kwa sababu vituo na zahanati zimefika kwenye maeneo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kingine tu nilikuwa nataka kusema, nilikuwa nasikiliza sana, jana nimesikiliza ile speech ya Mwalimu huwa inarudiwa ya yule mposaji. Kwanza ilikuwa ni baada ya Aridhio TBC. Pamoja na kutamka TBC, niseme tu, Mwenyezi Mungu aiweke mahali pema Peponi roho ya Marehemu Marin Hassan Marin kwa sababu alikuwa ni mtangazaji mahiri sana.

Mheshimiwa Spika, kile kipindi kilionyesha Mwalimu Nyerere akisema, yule kijana mposaji; ile kuzomewa huyo, huyo, huyo, eeh, huyo! Mimi nilikuwa natafakari sana, nikasema Mheshimiwa Waziri Mkuu zile kelele za huyo, huyo, huyo, tumeshinda. Kwa sababu kuna mambo mengi ambayo tusingeweza kuyafanya kama Mheshimiwa Rais asingeziba masikio. Tumenunua ndege, bwawa la kufua umeme, reli inakuja na mambo mengine mengi kweli. Kama angeweza kusikiliza zile kelele za huyo mkamate, huyo hawezi, huyo anadondoka, tusingeweza kufika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba tuendelee, tusonge mbele kwa sababu bado hatujafika. Kwa hili nataka tu niseme kwamba namwombea Mheshimiwa Rais wangu, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, kazi aliyoifanya ni kubwa sana, hatuna sababu kwa sababu mimi najua kabisa ndugu zetu hawa wako kwa ajili ya kukosoa yale mambo ambayo hatuwezi kufanya, lakini yale mambo yaliyofanyika hakuna sababu hata ya kumpeleka Mheshimiwa Rais akaanza kuomba kura. Anaomba kura wapi?

Mheshimiwa Spika, wananchi wameziona kazi; anaomba kura za nini tumsumbue barabarani huko, azunguke akaombe kura! Tunamwacha, sisi tupambane kwenye Majimbo huku, nafasi ya Rais ibaki yule yule. Ninyi njooni kwenye Majimbo tupambane, lakini Rais abakie yule yule kwa sababu anatosha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho kabisa, wewe ni mtani wangu, najua utarudi tu, mimi nitakutambikia, wewe usiwe na wasiwasi, hakuna mtu atakuja pale, wewe tulia tu. Wewe chukua fomu, rudisha, njoo endelea kuandaa Bunge linalokuja kwa sababu wengi wetu tutarudi kutokana na kazi kubwa ambayo Serikali hii imeifanya na wananchi wameiona. Kwa hiyo, hakuna mpinzani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ambalo nilitaka nizungumze ni suala la Corona. Mheshimiwa Rais alionesha mfano mzuri sana wa imani na watu wameendelea kusali. Nataka niwaambie, tuendelee kusali lakini pia huku tukichukua tahadhari, tukiwafuata viongozi wetu wataalam wanatuambia nini? Ukisali na huku ukamwomba Mwenyezi Mungu na ukachukua tahadhari, huwezi ukawa juu ya mtu ukasema wewe jirushe tu Mungu atatuma Malaika, hapana. Ni kwamba unashuka taratibu na Mungu atakusaidia, utashuka kwenye huo mti. Kwa hiyo, tuendelee kusali, tumwombe Mwenyezi Mungu huku tukichukua tahadhari zile ambazo tunaelekezwa na viongozi wetu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Profesa Mama Tibaijuka yeye amezungumza kuhusu tiba asilia nikamkumbuka, mimi ni wifi yangu. Ukienda kwa shemeji zangu kule wana dawa moja hivi; ukiumwa Malaria hawakupeleki hospitali. Nikapima, wanakwambia wewe tulia, kuna dawa moja inaitwa Omushana. Kwa hiyo, nikamkumbuka, nikasema siyo ajabu ameshaanza kunywa Omushana ile ambayo huwa inapandisha immunity zile ambazo zinasaidia kupambana na maradhi. Ila kitu kikubwa ni kuwasikiliza wataalam wetu, Mheshimiwa Rais ameshakabidhi Mheshimiwa Waziri Mkuu. Mheshimiwa Dada Ummy ambaye anafanya kazi nzuri sana pamoja na Mheshimiwa Dkt. Ndugulile tuendelee kuwasikiliza.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sijagongewa kengele ya mwisho kabisa kuhusu ushirika; pale Manyoni tumeletewa barua watu wamezuiwa kuuza mazao yao; zile Dengu, Ufuta na nini, eti mpaka wakauze kwenye Chama cha Ushirika. Hebu ushirika wajipange kwanza...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mungu akubariki.
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi nitoe mchango kidogo kwenye hotuba hii ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Kwanza kabisa nianze kwa ku-declare kwamba na mimi ni moja kati ya wale wasanii ambao tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwamba sasa tunatambulika rasmi kwenye Wizara. Lakini nimesimama kwa ajili ya mambo mawili tu au matatu.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kumpongeza Mheshimiwa Rais na kumshukuru kwamba nilipoingia mwaka 2005 ndani ya Bunge hili, kwa kweli kulikuwa hakuna namna yoyote au neno lolote kuanzia kwa Waziri au Mbunge aliyezungumzia suala la sanaa. Lakini tulilianzisha na hatimaye Serikali ya Awamu ya Nne ikaweza kulitambua na kuanza kulifanyia kazi. Nitoe pole sana kwa wasanii wengi ambao wamekuwa kwanza ni maarufu kwa kujitahidi wao wenyewe, wamekuwa ni maarufu kwa kufanya kazi katika mazingira magumu, lakini na wengine ambao wana vipaji wameshindwa kuendelea kutokana na taratibu ambazo hazikuwa zinatambuliwa rasmi katika mfumo ambao sasa hivi umewekwa na Rais huyu wa Awamu ya Tano kwa kweli nampongeza na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake kwa kasi kubwa ambayo wameianza sasa inayoonekana. Ninapongeza kwamba ameweza kuzindua tamasha la filamu la Kimataifa pale Arusha ambalo naamini tamasha lile ni mwanzo mzuri utakaowapa fursa wasanii wetu kutangaza kazi zao ndani na nje ya nchi. Kwa hiyo, ninakupongeza sana Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niseme jambo moja, Mheshimiwa Waziri kwamba sanaa haikuwa na Wizara ambayo tumeililia pamoja na wasanii wenzangu ambao tuko ndani ya Bunge hili. Kwa umoja wetu tuliweza kushirikiana kulilia ili sanaa hii sasa iweze kupewa nafasi katika Wizara. Umepewa nafasi sasa, hebu ninaomba kwa sababu inaonekana kuna wasanii ambao wanaonekana labda ni wakubwa sana, wengine ni wadogo sana au kuna ubaguzi. Mimi nataka niwashukuru sana wale watu, vyombo mbalimbali na taasisi mbalimbali ambazo ziliwasaidia wasanii wetu hadi kufikia hapa walipo kwa sababu Serikali ilikuwa haijatia mkono wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyo vyombo mbalimbali ambavyo vimekuza vipaji vya wasanii hata tukizungumza Diamond, Diamond amepitia kwa ndugu Ruge kwa kweli tunawapongeza, mimi binafsi kuna wasanii wengi wamesaidiwa hata tulikuwa na kina Saida Kalori walisaidiwa, wakakuza vipaji vyao. Ninapongeza vyombo hivyo kwa sababu walihangaika, ndugu Msama alijitolea kuanza kukamata kazi za wasanii ambazo zilikuwa zinaibwa, kwa sababu Serikali ilikuwa haijatia mkono wake pale, kwa hiyo mimi napongeza sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mzee King Kiki ambaye leo tunae hapa, wazee hawa wamepata taabu kubwa, wamehangaika, Serikali haikutia mkono kule kuwasaidia lakini wameweza kufika hapa na wametangaza pia kazi za sanaa na Taifa letu, mimi ninawapongeza wote.
Lakini Mheshimiwa Waziri, tunayo mashirikisho ambayo mashirikisho haya yako manne, kuna Shirikisho la Filamu lina vitengo vyake, kuna Shirikisho la Muziki lina vitengo vyake, kuna shirikisho la Sanaa za Ufundi na Shirikisho la Sanaa za Maonyesho. Ukienda kwa mfumo huu ukapitia mashirikisho haya, hii kuonekana kwamba wasanii sasa wanatengwa, nafikiri haitakuwa na mashiko maana yake hata sasa hivi sina hakika kama umealika viongozi wa mashirikisho haya, sana sana utakuwa umeita watu wachache kuja kuwawakilisha wasanii.
Kwa hiyo, ninaomba ufanye kazi na mashirikisho haya, wao watakueleza ni nini adha na wanahitaji kufanya mambo yapi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mashirikisho haya yatakusaidia katika mambo mengi, kwa mfano, msanii aliyepo Kigoma, Singida au Mtwara kuwe na branches kule ambazo wao watatambulika kule. Kwa sasa hivi msanii hawezi kukopesheka pamoja na kipaji alichonacho, pamoja na kazi nzuri aliyonayo hatambuliki, lakini anapokuwa ni mmoja kati ya wanachama ambao ni wanachama katika mashirikisho haya, ninaongea kwa kifupi kwa sababu yana mapana na marefu yake lakini yatasaidia sana. Kwa hiyo msanii huyu anaweza akakopesheka kupitia haya mashirikisho, lakini unaweza ukamtambua kupitia pia kwenye haya mashirikisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie suala la COSOTA. Ni kweli nilikusikia kwamba unasema COSOTA ihamie kwenye Wizara yako na sisi tutakuwa na furaha ikihamia kule. Sasa hivi inakusanya mrahaba kwenye vyombo mbalimbali redio, tv, magazeti na kila kitu, lakini nani anasimamia kujua msanii fulani, kuna chombo gani ambacho kinaonesha kwamba wimbo wa mtu fulani umepigwa mara ngapi, gharama yake ni kiasi gani na anatakiwa alipwe nini? Kwa hiyo, tunaomba sana kama COSOTA itahamia kwako tunaamini kabisa utaweza kusimamamia.
Mheshimiwa Naibu Spika, bado kuna suala la mikataba la uuzwaji wa kazi za wasanii. Nadhani kwenye mashirikisho haya uweke wanasheria watakaosimamia kazi hizi na mikataba ya wasanii. Wasanii wengi anapewa shilingi milioni 10 anaenda anagawana na wenzake inatoka lakini anaendelea kutajirika yule msambazaji. Simamia haya mashirikisho yatakusaidia kusaidia wasanii hawa waweze kupata kazi zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kuna mmoja amesema kazi za nje. Hebu pigeni kazi za ndani lakini bado na zile zinazouzwa mitaani, sisi tunalipa sticker, tunalipa TRA lakini kuna kazi hazina sticker, zinaharibu soko la wasanii hapa nchini. Tunaomba jamani mipaka, akitaka kuuza basi waende TRA na wao wakalipe zile sticker na utoaji wa sticker uende mpaka mikoani. TRA wapunguze ule mlolongo, waende mikoani ili wasanii wote waweze kupata huduma kule walipo. Hakuna haja ya mtu kutoka Mtwara, Kigoma au Bukoba, aende Dar es salaam kwa ajili ya ku-register kazi yake. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ninaamini kabisa suala hili utalisimamia barabara.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala jingine nakuomba ujenge Kituo cha Sanaa. Kituo kikubwa ambacho wasanii wote watapatikana pale, watafanya kazi pale, hata kama mtu anataka kufanya nendeni kwenye nchi za wengine mkaone ni namna gani ili hata kama watu wanataka kwenda kumuona msanii fulani, wanajua tukienda kwenye kituo fulani leo kuna maonesho haya, kesho kuna maonesho haya. Lakini na wale wanaotaka kufanya filamu zao kunakuwa na eneo kubwa ambalo linakuwa limetengwa, ardhi tunayo, lakini siyo vibaya hata tukajenga kukawa na kijiji cha wasanii kule, maana sasa hivi ukweli ni kwamba wasanii bado ni maskini sana, tunalo Shirika letu la National Housing, tupeni ardhi, tujenge, dhamana ni kazi zetu, tutalipa! Ili wasanii wapate maeneo mazuri ya kuishi, tupeni ardhi. Mimi ninakutakia kheri, ninaamini na ninakuamini, naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuwateua Mheshimiwa Profesa Muhongo na Naibu wake Dkt. Kalemani, tuna imani nao na tunawaombea pia tutawapa ushirikiano. Pamoja na pongezi hizo pia tunawapongeza sana Viongozi Wakuu wa Wizara hii, Katibu Mkuu na Watendaji wote wanayoyafanya katika kutekeleza majukumu yao vizuri sana, hongereni sana na naunga mkono hotuba.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi nina mambo mawili ya kuomba:-
(i) Mradi wa umeme wa upepo Singida tafadhali tunaomba sana mradi huo uanze, tuna makampuni mengi yanayotaka kuwekeza huko na mengine yalishafanya tathmini ya fidia kwa wananchi na wananchi wanasubiri kulipwa fidia. Hii itasaidia sana kutuliza maswali.
(ii) Wachimbaji wadogo wa Sekerike, Hondo na Samsaru wanaomba wapatiwe umeme, pia kuna wawekezaji ambao ni ASHANTA wamezuia maeneo ambayo hawayafanyii kazi yoyote, hivyo inaleta mtafaruku sana kwa wachimbaji wadogo. Naomba Wizara iliangalie ili itende haki ya kuwapa wananchi walio tayari.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi naomba nipongeze Kamati
zote kwa taarifa walizowasilisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nina machache, kwanza ninapongeza kwa maendeleo
yote ambayo yamepatikana tangu uhuru mpaka sasa, maana kwa kweli tumepiga hatua
kubwa sana kwenye upande wa miundombinu ya barabara, lakini bado hata kwenye matumizi
ya simu za mikononi. Sasa hivi watu wanapata redio, mawasiliano na taarifa kwenye simu za
mkononi, yote ni maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nina mambo yafuatayo:-
Kwanza, nilikuwa naomba sana Wizara ihimize taasisi zinazohusika, kwamba kwenye kasi
ya maendeleo na wenyewe wakimbie. Kwa mfano, mji unapokua, miundombinu ya umeme
ambayo inakuwa imewekwa, TANESCO hawaendani na ile kasi. Utakuta maeneo watu
wameshajenga, hakuna transfoma hakuna nini, kwa hiyo, nilikuwa naomba sana waendane na
kasi ya maendeleo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna suala la hawa wakandarasi wa REA. Pale Mkalama,
kuna vijana 40 ambao wanadai hela zao kwa muda mrefu, miezi mitatu sasa hawapewi.
Mheshimiwa Waziri nilikuwa naomba tusaidie kuhusu mkandarasi yule, wale vijana walipwe
maana anawakimbia mpaka sasa hivi hataki kuwaona.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nimepata taarifa kutoka kwa wananchi wanaolima
vitunguu kule Mkalama, kwamba kuna mtafiti mmoja amepewa leseni ili akatafiti madini
yanayopatikana pale na awaondoe wale wakulima wanaolima vile vitunguu. Ninaomba suala
hili lisitishwe mara moja, wananchi waachwe, waendelee kulima zao la vitunguu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna jambo lingine, Mheshimiwa Waziri nakushukuru
ulifika Singida ukaenda Tumuli ukakuta kuna wachimbaji wadogo wananyanyaswa na
wanadhulumiwa, ukaagiza tatizo lile litatuliwe, lakini mpaka sasa hivi bado wale wachimbaji
wadogo hawaelewi hatma yao. Kwa hiyo, nilikuwa ninaomba sana ufike pale ili uweze
kuwasaidia wale vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, yangu ni hayo tu. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi kwa kazi nzuri sana inayofanywa na Waziri pamoja na Naibu Waziri, bila kuwasahau Katibu Mkuu na watendaji wote, naomba nitoe ushauri kidogo kuhusu suala ambalo ninaona; kuna utata na linatesa sana wazazi wa watoto wanaohitimu kidato cha nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtihani wa Taifa wa kuhitimu kidato cha nne hufanyika kila mwezi Oktoba ya mwaka, matokeo ya kidato cha nne hutoka kati ya Januari na Februari, lakini wanaopaswa kuendelea na masomo ya kidato cha tano wanasubiri hadi mwezi Julai. Hivyo, mtoto huyu ana miezi takribani nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakika hii ni mateso sana kwa watoto kusubiri na wazazi kuwalinda watoto hawa ili wasije wakaingia kwenye kujifunza mambo yasiyofaa na kudumaza ari na moyo wa kusoma na uwezo unapungua. Hali hiyo, huwapelekea wale wenye uwezo kuwapeleka watoto wao pre-form five kitu ambacho kwa wasio na uwezo kinawanyanyapaa.

Ushauri wangu matokeo ya kidato cha nne yanatoka Januari ili kubaini waliofaulu, watoto wanaofaulu kuanzia alama “D” one to three, wapelekwe JKT kwa muda wanaosubiria kuanza kidato cha tano mwezi wa saba. Hivyo, kuanzia Februari hadi Juni. Wakishahitimu watapata muda mdogo tu wa kukaa nyumbani na hivyo kuendelea na masomo vizuri. Hivyo itaondoa JKT ya kidato cha sita haitakuwa na haja ya kuwepo. Utaratibu wa kuwapata vijana kwenda kwenye Majeshi yetu unaotumika utabadilika na badala yake watapata walioenda JKT moja kwa moja. Mfano Jeshi la Polisi, Magereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kama utaratibu wa kuwapeleka Jeshi la Kujenga Taifa litaonekana halifai, basi itafutwe namna yoyote kuhakikisha muda wa kuanza kidato cha tano unasogezwa ili waanze Mei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii lakini naomba tu kwanza nikupongeze kwa kazi kubwa unayoifanya na nataka nikuhakikishie kwamba Mungu yupo upande wako, upo hapo kwa makusudi ya Mungu na ataendelea kukulinda, sisi tupo pamoja na wewe. Kupitia Mwezi huu Mtukufu naamini wengi wanakuombea kwa hiyo tunaomba Mungu aendelee kukubariki, songa mbele mwanamke mwenzetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nimpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu amerejesha imani kubwa sana kwa Watanzania. Ninasema haya kwa sababu nidhamu makazini imerejea, watu wanatulia maofisini, watu wanawahi maofisini na wanafanya kazi wanayostahili kulipwa mshahara huo, kwa hiyo nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na watendaji wote tunawaamini, tunaomba muendelee kuchapa kazi lakini naomba sana mtembee kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais wakati anaomba kura na wakati analihutubia Bunge, nataka nimpongeze kwa sababu anatembea kwenye yale maneno yake aliyokuwa anayasema. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri sijaona kipengele kimojawapo ambacho Mheshimiwa Rais alikuwa anazungumza wakati akiomba kura na wakati anahutubia Bunge. Alizungumza sana kuhusu watu wa kima cha chini, wafanyabiashara ndogo ndogo, kina mama lishe, wauza nyanya, viazi, vitunguu, boda boda na wengine wote, nashangaa ametoka kwenye mstari hata hao boda boda sasa naona amewapandishia tozo badala ya kutembea kwenye maneno ambayo Mheshimiwa Rais aliongea.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alisema mgambo watatafuta kazi nyingine ya kufanya lakini hotuba ya Waziri haionyeshi kama mgambo watatafuta kazi nyingine ya kufanya kwa sababu wale mama lishe au wafanyabiashara ndogo ndogo kwenye ushuru mdogo mdogo ambao Mheshimiwa Rais alisema usio na maana utaondolewa hatujasikia, nilidhani TAMISEMI wangeleta lakini halikuonekana hili na bajeti hii iko kimya. Naomba Waziri atamke jambo kwa ajili ya wafanyabiashara hawa wadogo wadogo hasa akina mama lishe, wauza nyanya, vitumbua, wanaofukuzwafukuzwa na mgambo. Ukienda Singida pale utakuta kuna miwa, nyanya, vitunguu, karanga, tunaomba utulivu wa hawa watu ambao walisubiri sana kauli ya Mheshimiwa Rais itekelezwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli wafanyabiashara hawa wanategemewa na watu wengi sana. Kuna watu ambao ni wafanyabiashara wanategemewa na watoto wao, wazazi wao lakini wale wanaofanya kazi kwenye viwanda wenye vipato vya chini wanategemea kupata huduma kutoka kwa hawa mama lishe ambao wanatoa huduma kwa bei nafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nizungumzie suala la Mkoa wangu wa Singida. Waziri amesema kwamba Mkoa wa Singida ni miongoni mwa mikoa ambayo uchumi wake bado upo chini sana lakini nashangaa sana kwamba mtoto ambaye amekonda ndiye ambaye bado unaminywa. Sasa sielewi Mkoa wa Singida tumekosa nini? Ametaja reli ya kati ambayo inaenda kujengwa, akataja michepuo ya reli zote lakini akaacha kuitaja reli inayotoka Dodoma - Manyoni - Singida na reli ile ndiyo iliyokuwa inawasaidia sana wananchi wa Mkoa wa Singida. Mkoa huo unategemea uchumi wake kupitia reli ile.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi ni wakulima wazuri sana wa zao la alizeti, tunategemea uchumi wa viwanda, lakini tuna mifugo, tuna kuku, tunalima viazi vitamu ambavyo hakuna mkoa mwingine unaolima viazi vitamu kama Mkoa ule wa Singida. Tuna vitu vingi ambavyo tunategemea kuvisafirisha kwa kutumia reli ile. Kwa hiyo, naomba sana aiingize kwenye hiyo michepuo ya reli nyingine alizozitaja, vinginevyo anawavunja moyo wananchi wa Mkoa wa Singida ambao wao wameinuka kwa kasi kubwa sana katika kujiletea maendeleo na wamejitahidi sana mpaka sasa hivi na nawapongeza. Kwa hiyo, naomba asiwavunje moyo, vitunguu vilivyo bora Afrika Mashariki vinatoka Singida. Kwa hiyo, namuomba sana reli hii aiweke katika list yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nizungumzie pia miradi ya zamani. Kuna miradi ambayo imekuwa ikitengewa fedha, inaanzishwa lakini matokeo yake inaachwa, fedha zile zinakuwa zimepotea. Tunafika hapa tunatenga tena fedha tunapeleka kwenye miradi mingine, hivi hatuwezi tukaanza na kitu kimoja tukakimaliza ili twende kwenye kitu kingine? Kwa mfano, ukienda Mkalama utakuta kuna mabwawa ambayo yalishaanza kuchimbwa, miradi ile haikukamilika imeachwa takribani miaka kumi sasa ipo tu na fedha zilitumika. Kuna bwawa la Mwanga, Mwangeza, Msingi, ukienda Iramba kule Urugu na maeneo mengine miradi mingine imekuwa kama magofu. Naomba fedha hizi ziende kukamilisha miradi hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la wakulima kuna ruzuku lakini wavuvi mbona wametengwa hakuna ruzuku yoyote? Hebu ondoeni kodi kwenye vifaa vya uvuvi. Mheshimiwa Rais alisema anatamani kuona meli ya uvuvi ambayo ni kiwanda kuanzia mwambao Tanga, Dar es Salaam, Lindi mpaka Mtwara. Hebu ondoeni ushuru kwenye mafuta yanayoendeshea vyombo vya uvuvi ili muwasaidie na wenyewe maana hawana ruzuku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kuzungumzia tozo kwenye utalii, wengi wamezungumza. Hivi mnataka Kenya waendelee kutupiga bao kwamba ukifika Kenya utauona Mlima Kilimajaro! Mkishaongeza na hiyo tozo ambayo mnaiweka watafika Kenya wataona Mlima Kilimanjaro wataondoka zao. Halafu tunasema tunaongeza ajira kwa vijana, hapa tunawaminya wale ambao wapo kwenye sekta ya utalii. Kwa hiyo, naomba sana kwenye eneo hili na lenyewe Mheshimiwa Waziri mliangalie.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu na suala la mikopo upande wa wajasiriamali wanawake. Amezungumza mwenzangu, akina mama wanazalilishwa sana, wengine wamevunja ndoa zao kwa sababu asubuhi anakuja kunyang‟anywa TV na mume wake anashuhudia, anaambiwa TV ikiondoka, friji ikiondoka ongozana navyo, hakuna kurejea hapa nyumbani. Kwa hiyo, naomba sana suala hili liangaliwe na hizi benki zinazohudumia akina mama ni lazima ziende kwenye mikoa mingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii. Na mimi niungane na wengine kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya siku ya leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichukue nafasi hii kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Singida kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa namna ambavyo aliamua kwa vitendo kuleta Makao Makuu ya Serikali hapa Dodoma. Kwa kweli ni uamuzi wa kishujaa na busara, nampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu yeye ndiye aliyeongoza jahazi la Mawaziri kwa maana ya Wizara zote kuja hapa. Nimpongeze sana Mheshimiwa Jenista na Ofisi yake maana yeye ndiye aliyetangulia kufungua mlango kumpokea Waziri Mkuu. Kwa kweli pongezi sana Mheshimiwa Jenista kwa kuratibu zoezi hili na kuhakikisha Wizara zote zinakuja hapa
Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza haya kwa sababu Dodoma ni pacha na Mkoa wa Singida. Kwa hiyo, pacha wetu akipata neema na Singida tunapata neema kwa maana ya kwamba Wizara zote na watu wengi watakaoishi hapa Dodoma watatumia bidhaa kutoka Singida. Kwa hiyo, sisi wana Singida tumejiandaa kuleta mazao mbalimbali kwa maana ya kuku, karanga, viazi, vitunguu na mazao mengine mengi pamoja na mafuta mazuri sana ya alizeti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri kidogo kwamba mara nyingi Makao Makuu ya Serikali jengeni Mji uwe Makao Makuu ya Serikali. Naomba ile miradi mikubwa ya uwekezaji leteni kwenye Mikoa yenu iliyo jirani ukianzia Singida ili Mji huu ujengeke kama Mji wa Kiserikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niwapongeze Mawaziri wote. Mawaziri safari hii mmekuwa wanamgambo kweli kweli. Mmeweza kuchapa kazi hamjakaa maofisini. Sisi wenzenu tunataka tuwaambie, mnapofika mikoani hata wale watendaji wenu waliopo kule hakika wanapata hamasa ya kufanya kazi. Pia wananchi wanapoona Mawaziri mnatembelea miradi na kuangalia changamoto mbalimbali hiyo tunajijengea imani kwa wananchi kwamba Serikali yao inawajali. Pongezi sana Mawaziri wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru hivi karibuni Waziri wa Nishati na Madini alikuja Singida kufungua Mradi wa REA III. Kwa kweli napongeza sana na tunawaomba wale wakandarasi wakatimize sawasawa na mkataba unavyosema ili wananchi waendelee kunufaika na mradi huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyoileta hapa nataka kusema iko sahihi kabisa, lakini nataka kushauri katika eneo moja tu. Eneo hilo ni kutokana na diplomasia ya kiuchumi inayofanywa na Mheshimiwa Rais wetu. Marais waliopita wamefanya lakini
na yeye amefanya diplomasia kubwa sana maana tumeshuhudia viongozi wakuu mbalimbali wa nchi wakitembelea nchi yetu, kwa kweli ninampongeza lakini tumeshuhudia mikataba kwa maana ya makubaliano (MoU) zikisainiwa pale Ikulu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kuuliza ni nani anayefuatilia makubaliano haya kwa sababu tunahitaji kupata mrejesho kwamba ilisainiwa 20, 60 au mingapi na imetekelezeka mingapi? Pamoja na kwamba tumeona kuna mingine imeshaanza, lakini kwa ushauri wangu kwa sababu nina mfano halisi, tangu Rais wetu ameingia naomba nisitaje Marais au wakuu wa nchi ambao wameshakuja hapa kwetu na kusaini mikataba mbalimbali ni tisa, ni mingi. Kwa hiyo, nashauri kuwe na chombo maalum cha kitaifa ambacho kitaundwa kiwe chini ya Kamishna ambaye ni mbobezi katika masuala ya uchumi na diplomasia. Chombo hiki kiwe na wanasheria, wanadiplomasia, wachumi na kadhalika ili waweze kukaa kuainisha MoU hizi na kuhakikisha zinapelekea kwenda kwenye mkataba unaotekelezeka. Kamishna huyu awe anaweza kucommunicate na taasisi zote zinazohusika kutokana na MoU hizo au makubaliano hayo ili kuleta matokeo chanya ambayo yamekusudiwa na viongozi wetu husasan Rais wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza hayo kwa sababu kabla ya awamu hii alikuja Rais kutoka China na viongozi wengi pamoja na wafanyabiashara na Rais wetu akaenda. Alipofika hapa wakaingia MoUs nyingi lakini utekelezaji wake mmoja tulifika pale Beijing China wakatuambia kwamba kulikuwa na makubaliano ya ndege ya China kuja Tanzania kuleta watalii, lakini hakuna aliyeweza kujibu suala lile hatimaye ndege ile ilihamia Kenya. Hii inatia uchungu na ndiyo maana nimeshauri kuwe na chombo maalum kitakachosimamia makubaliano hayo kupelekea kwenye utekelezaji unaoleta matunda chanya katika taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, isije tukaishia tu watu kupiga picha na kumwaga wino, ni lazima tuwe na mkakati huo. Pia kuwe na library ya kutunza mikataba au makubaliano hayo. Ni nani anaweza akatuambia, je, kuna maktaba inayotunza, iko mingapi? Napenda nijue kwa miaka mitatu au minne awamu iliyopita na hii, je, ni mikataba au makubaliano gani ambayo yamefikia kwenye utekelezaji? Naomba sana hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa kumalizia, tulipotoka ni mbali Taifa hili na Mungu wetu amekuwa akitupenda Watanzania, amependa sana Taifa letu. Naomba kusema anayefikiri na kudhani amesimama na aangalie asianguke. Kwa sababu ufalme ukifitinishwa hakuna atakayebaki salama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba anayedhani amesimama na aangalie asianguke. Tusije tukawa kama wale wajenga mnara wa Babeli kila mtu akazungumza lugha yake kwa sababu walitaka kumpandia Mungu kichwani ndio maana Mungu akawasambaratisha. Naogopa Taifa hili tusije tukasambaratishwa kwa kunena na kutaka kupanda kwenye maeneo ambayo hakika sio nafasi yako. Anayedhani amesimama na aangalie asianguke. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namtia moyo Rais wangu, endelea kufanya kazi, haukuja kimakosa maana kila utawala ni maridhio ya Mwenyezi Mungu. Fanya kazi tupo pamoja, kuwa mnyenyekevu mbele za Mungu na Mungu atakuongoza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati fulani niliwahi kusema kuna watu humu ndani wako kama hali ya hewa ya Dar es Salaam. Dar es Salaam jua litawaka leo, kesho ni mafuriko, leo ni mafuriko kesho ni kipupwe. Kwa hiyo, kuna watu ni vigeugeu, leo watasifia jambo, kesho watalibeza, leo watalalamikia jambo, kesho watalibeza. Rais wetu kama nyumba inavuja tia gundi, tia nta, endelea kuchapa kazi kwa maana mvua haiwezi kuacha kunyesha. Naomba nimtie moyo Rais wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, narudia kusema kwamba naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na sisi Wanasingida tumejiandaa sawasawa, michango mingine nitachangia kwenye Wizara zinazofuata. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kuchangia. Wakati naongea, naomba ni-declare kwamba mimi pia ni msanii wa nyimbo za injili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu mwaka 2005 nilichaguliwa kuingia ndani ya Bunge hili na nilipoingia ndani ya Bunge hili, hapakuwa panazungumzwa habari za sanaa ndani ya nyumba hii, lakini mpaka sasa hivi ni hatua kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka wakati huo kabla sijawa Mbunge tulikuwa tumeanzisha uanaharakati kwa ajili ya kutetea haki za wasanii. Kwa hiyo, nilipoingia kwa kweli niliendeleza na ndiyo maana mpaka leo hii tunamshukuru Mheshimiwa Rais ambaye ameweza kugundua umuhimu na kuingiza sanaa kwamba ni mojawapo ya Wizara maalum kabisa. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza sana Mawaziri, Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe pamoja na dada yangu kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya na Katibu Mkuu. Tumeiona kwa sababu sisi tunaelewa tulipotoka mpaka hapa tulipo. Kwa hiyo, nawatia moyo muendelee kufanya kazi pamoja na kwamba bajeti yenu kwa kweli hairidhishi, lakini ninaamini kwa utendaji wenu mzuri hakika mta-perform vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi Singida. Naomba nichukue nafasi hii kupongeza sana timu yangu ya Singida United ambayo imeweza ku-perform vizuri na kuweza kuingia ligi kuu. Nampongeza sana Rais wa Singida United, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Mwenyekiti wa Singida United, Ndugu yetu Yusuph Mwandami na viongozi wote wa Singida United walioisaidia ikafikia hapa ilipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe tahadhari na tangazo moja kubwa sana kwamba Dar es Salaam tunaomba mjiandae, nyang’anyaneni kombe hili, yoyote atakayepata tutunzieni. Singida sisi tunaenda kubaki na kombe hili, hamtaliona tena huko. Natoa salamu hizo.

Yah, lazima libaki Singida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nishukuru sana TFF. Namshukuru Rais wa TFF, Ndugu Malinzi, Katibu Ndugu Mwesiga na Ndugu Salum Madadi ambao wamekuwa karibu sana na sisi kutusaidia na kutuelekeza ni namna gani tunajenga uwanja wetu uweze ku-qualify ili mechi iweze kucheza Singida. Na sisi Chama cha Mapinduzi tumejipanga, naipongeza Kamati yangu ya Siasa ya Mkoa ya Chama ambayo wamesimama kidete kuhakikisha uwanja ule unakamilika. Nawapongeza sana, big up sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wadau tushirikiane kwa sababu Kanda ya Kati hakuna timu nyingine ya Ligi kuu zaidi ya Singida United, tuisaidie ili kombe liendelee kubaki Makao Makuu ambayo ni Kanda ya Kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, pia nisisahau kumpongeza Alphonce Simbu, kijana ambaye anatoka Singida, ametupa heshima kubwa sana kwa kazi nzuri aliyoifanya na kupata medali ya dhahabu na alipoenda London Marathon ameshika nafasi ya tano, tunamtia moyo, ame-improve, tunaamini mwakani atashika nafasi nzuri na tumtakie heri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze, nimesha-declare interest, nataka niseme kuhusu jambo moja ambalo lipo mitaani sasa hivi, hasa kwenye tasnia ya filamu. Vijana wapo mitaani hawana kazi, filamu zao ambazo wamezicheza zimebaki kwenye makabati, siyo kwamba hazina ubora, lakini kuna tatizo kubwa sana ambalo nashukuru sana Wizara ilishaanza kushughulikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana muelewe wazi kwamba taratibu zinazotumika siyo sahihi kwa sababu ushindani umekuwa ni mkubwa. Kazi za nje zinazoingia ndani, tena zinatafsiriwa kiswahili na kazi hizi za nje zikija zikitafsiriwa kiswahili, watu wa nchi za Magharibi wanakuja kununua kwa sababu wanazungumza kiswahili. Kwa hiyo, kazi zetu sisi hazipati soko kwa sababu ya bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za ndani kutengeneza filamu moja inatumia zaidi ya shilingi milioni 18. Kuanza tu kuandika andiko kwenda kwenye Bodi ya Filamu ni shilingi 500,000, urudi COSOTA, sijui ikaguliwe, ukiigiza, maudhui, maadili, yote ni hela mpaka COSOTA, uende TRA ni hela. Process hii ni ndefu na ni hela nyingi, kwa hiyo, msanii huyu auze shilingi ngapi? Ndiyo maana unakuta soko za filamu hizi zinakuwa hazinunuliwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, hizi kazi za nje wala hakuna haja ya kuwafungia watu. Wekeni utaratibu na wafuate taratibu wanazofuata hawa wa kazi za ndani. Wakishafuata, hakuna tatizo kwa sababu bei itakuwa ni moja na kazi zitanunuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie, Tanzania ni nchi ya pili kwa ubora wa kazi za filamu ikitanguliwa na Ghana, lakini kwa sababu ya gharama za uzalishaji, ndiyo maana unakuta kazi hizi hazipati wateja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumze suala la Sera ya Filamu. Sera ya Filamu kama tutaipitisha hapa itakwenda kurekebisha sheria na taratibu ambazo zitaweza kuwabana hata wale maharamia. Kwa sababu Sheria ya COSOTA sasa hivi ilivyo, mtu akikutwa na kazi haramu za shilingi bilioni moja, akipelekwa Mahakamani ni shilingi milioni tano, lakini kazi ni shilingi bilioni moja au jela miaka mitano. Obviously yule mtu yupo tayari kulipa gharama hizo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe namwamini sana kaka yangu, atakwenda kushughulikia hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado nashauri, kwa sababu tuna chuo chetu cha Bagamoyo lakini hatuna Chuo cha Filamu, hebu naomba hilo, bado vijana hawa hawawezi kukopesheka. Nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri, wasanii hawa wapo takriban milioni tisa Tanzania. Afanye research ataona, ni ajira na ni kiwanda kikubwa sana kama tutawawekea mazingira mazuri ambayo Mheshimiwa Rais wetu amekusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Sera ya Filamu, Mheshimiwa Waziri aende BASATA akashirikiane nao wampeleke kwenye yale mashirikisho manne ambapo kuna Shirikisho la Filamu, Shirikisho la Kazi za Ufundi, Shirikisho la Muziki na Shirikisho la Sanaa za Jukwaani. Akienda kule kuna vyama, ndiko wasanii walipo ili wawawezeshe BASATA waweze kufanya kazi na mashirikisho haya kuwasaidia Watanzania wote. Maana tukisema kazi za ufundi; wapo vinyago, wapo akina tingatinga, wapo wachoraji, kuna waandishi na watu wengine, ni kiwanda kikubwa sana! Naomba sana Mheshimiwa Waziri aende BASATA akashirikiane nao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba tu nimalizie kwa kusema kwamba, hebu niwapongeze wale wadau wote ambao wamekuwa wakiwasaidia wasanii. Nianze na Ruge Clouds, Msama; wote hawa ndio wamehangaika na wasanii kufika hapa. Nakumbuka wakati tunaanza sanaa, Ruge alianza na Clouds FM kwenye chumba kimoja; lakini wasanii tulikuwa tunaenda kujibanza pale. Ameendelea kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu Serikali iwe inawaangalia watu hawa ili muwasaidie waendelee kuwasaidia wasanii. Mwangalie Msama anavyohangaika kukamata kazi za wasanii, anaishia tu kuwapeleka Polisi, hakuna sheria, hakuna nini. Kwa hiyo, naomba washirikiane na wadau hawa ili waweze kuwasaidia wasanii. Kwa mfano,...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, Tasnia ya Sanaa za Ufundi ndio yenye ushiriki mkubwa wa Wasanii kuliko sanaa nyingine nchini Tanzania. Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na BASATA 2006, idadi ya wasanii nchini ni milioni sita; zaidi ya milioni nne kati ya hao ni wale wanaojishughulisha na sanaa za ufundi wakiwemo, wachongaji, wachoraji, wachoraji katuni, tingatinga, wasusi, wabunifu wa mitindo, walimbwende na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, tafiti mbalimbali ikiwemo ya (WIPO) Word Intellectual Property Organization 2012), pia zinaonesha ni kiasi gani tasnia hii inachangia kwa kiasi kikubwa kwenye ajira na pato la Taifa kuliko hata madini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mchango huo kwa Taifa, sanaa hii haipewi kipaumbele na Serikali, hivyo kudumaza maendeleo yake. Changamoto zifuatazo ni baadhi ya vikwazo vya maendeleo katika tasnia hasa sanaa ya uchoraji. Sheria kandamizi hasa kuporwa kwa maeneo mfano, kama ilivyokuwa katika maeneo mengine ikiwemo Nyumba ya Sanaa, sasa kumetokea watu wanaotaka kupora eneo la wachongaji Mwenge, eneo ambalo lilikabidhiwa Chama cha Wasanii Wachongaji Tanzania (CHAWASATA) na Serikali ya Awamu ya Kwanza mwaka 1984. Kufuatia kuhamishwa kutoka barabara ya Ali Hassan Mwinyi Road (Zamani Bagamoyo Road) ili kupisha upanuzi wa barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa mshangao mkubwa wamejitokeza waporaji wenye nguvu za kifedha wanaoshirikiana na Kamishna wa Ardhi ili eneo lile lipewe watu wengine. Jitihada mbalimbali zimefanywa na chama cha CHAWATA ili kunusuru eneo hili lisiingie mikononi mwa wanyang’anyi ikiwemo kuomba msaada kwa vyombo vya umma ikiwemo BASATA ambao kwa barua yao ya hivi karibuni walisema jambo hilo haliwahusu.

Mheshimiwa Spika, naomba Wizara ituambie, nani anayehusika kufuatia hali hii tete ya sintofahamu. Hali ya amani katika Kijiji cha Mwenge Vinyago ni tete na wachongaji wasingependa kulazimishwa kuingia katika uvunjifu wa amani. Jamani, naomba suala hili lipatiwe majibu ili hali ya utulivu iendelee. Naomba sana Wizara hii ambayo iko chini ya Mwanasheria Dkt. Mwakyembe aliyebobea alisimamie hili kwa nguvu zote ili haki ya wachongaji hawa isipotee na wanamtegemea sana na wana imani na Waziri na watendaji wote.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine kubwa inayokabili fani ya uchongaji ni watu wa Maliasili na Utalii ambao wamekuwa wakizuia vinyago visipite Airport hata kama vina stakabadhi halali za TRA. Hali hii imedumaza soko la vinyago toka asilimia 59 hadi asilimia 15 kitu ambacho ni hatari na hii ni fursa kwa majirani zetu hususan Kenya. Kupitia Idara ya Sanaa, watu wa maliasili wameambiwa wakae nao ili kwa pamoja wajue na kufikia muafaka, lakini bila mafanikio. Inasikitisha sana.

Mheshimiwa Spika, pia kama ukifuatilia utendaji wa Mamlaka zingine hususan Tume ya Ushindani, bidhaa zote feki huwa zinachomwa zile zinazokamatwa tena hadharani, je vinyago vinavyokamatwa vinapelekwa wapi? Hatujawahi kuona vinateketezwa au kupigwa mnada ili kusaidia wenye mahitaji mbalimbali na kadhalika. Kuna tetesi kuwa, vinyago hivyo vinavyokamatwa pale airport hurudishwa Mwenge kwa mlango wa uwani. Naomba ukweli wa jambo hili na maelezo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kumbukumbu zangu kuna kauli aliyoitoa Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano kwamba COSOTA na BASATA ziunganishwe pamoja ili kuboresha utendaji kazi na kuwahudumia kwa ubora zaidi wasanii wote. Hii ni kutokana na COSOTA kushindwa kabisa kuwasaidia wasanii na kulinda kazi zao, kiasi kwamba zinaibiwa kila kukicha ilhali COSOTA wapo. Je, ni lini COSOTA na BASATA zitaunganishwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali au Wizara inatamka nini juu ya Msama Production ambaye yeye amekuwa akifanya kazi ya COSOTA ya kuzuia wizi wa kazi za sanaa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali haioni kuwa TRA wanapoteza mapato mengi sana kwa kutodhibiti wizi wa kazi za sanaa? Kwa sababu kudhibiti wizi huu na kazi zote zikauzwa kihalali, Serikali itapata na msanii atapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri kuwe na one stop center ya wasanii pamoja na vyama mbalimbali vinavyoanzishwa, lakini kuwe na mahali pamoja ambapo msanii au chama cha sanaa kingeweza kuripoti kwa maana sasa hivi Maafisa Utamaduni wako TAMISEMI, COSOTA iko Viwanda na Biashara na BASATA iko Wizara hii ya Habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hii kero na usumbufu wa TRA kuchelewesha kutoa sticker, kitu ambacho kimekuwa ni usumbufu mkubwa na kurudisha maendeleo ya wasanii wetu. Je, Serikali inalisaidiaje hili maana hizo ndizo kero za kutokana na kutokuwepo kwa one stop center ya wasanii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya nyuma COSOTA walikuwa wakiwalipa wasanii mirabaha ya kazi zao ambazo COSOTA hukusanya kupitia TV, Radio na kadhalika, lakini siku hizi hawalipi na kama wanalipa nadhani wanawalipa wasanii wachache sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kumnyang’anya COSOTA jukumu hilo na kutafuta chombo kingine kifanye kazi hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu COSOTA hawawezi, hata ukienda kuuliza wanadai kuwa mashine ya kufanya mahesabu ya mgao wanasema mpaka wapate mtaalam kutoka Uswisi. Je, hivi ni kweli hii nchi hakuna mtaalam wa hiyo mashine mpaka wamsubiri kutoka Uswisi? Kama ni kweli jambo hilo naomba kupatiwa majibu. Pia ningependa kujua hizo fedha zipo na ziko ngapi na ziko wapi? Hapa naomba majibu ya kina ama lah, nitashika shilingi na naweza kubaki nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba ya COSOTA imetoa muda wa kugawa hiyo mirabaha kwa wanamuziki lakini utaratibu huo haufuatwi. Katiba inasema mgao utakuwa Desemba lakini hautazidi mwezi wa Pili, lakini hadi sasa hawajalipa kwa muda mrefu sasa. Kauli yao ni mashine mbovu, mtaalam aletwe toka Uswisi! Jamani, Please!

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu warejee enzi za Mzee Steven Mtetewaunga alikuwa Afisa wa COSOTA, malipo yalikuwa mara mbili kwa mwaka mwezi wa Sita na Desemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasita sana kuunga mkono hoja. Naomba tu ieleweke wazi kuwa na mimi ni msanii wa muziki wa Injili Tanzania hivyo na-declare interest kuwa ni mdau wa sanaa ya muziki na nimesajiliwa COSOTA, BASATA na kadhalika.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatambua umuhimu wa Wizara hii na kazi kubwa sana na nzuri inayofanyika. Aidha, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa namna anavyoongoza Wizara hii kwa hekima na utulivu mkubwa . Pamoja na pongezi hizi naomba nimpongeze pia Jenerali Venance Salvatory Mabeyo kwa heshima kubwa aliyopewa na Mheshimiwa Rais, kwa kumteua kuwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, hongera sana. Kwa imani kubwa aliyonayo Rais wetu kwake ndivyo na sisi Watanzania tuna imani sana na yeye. Tunaamini ataendelea kushirikiana na viongozi wote walio chini yake na walio juu yake ili kuendelea kuwa na utulivu na amani tuliyo nayo nchini pamoja na usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi pia niwapongeze wanajeshi wote kwa kazi nzuri ya kulinda mipaka ya nchi yetu, hakika tunawapongeza kwani tunatambua kazi kubwa waliyonayo. Wakati wengine tunaendelea na shughuli zetu wao wakiwa katika shughuli nzito ya kutulinda wakati wengine tukiwa tumelala, wao wakiwa macho kutulinda. Hakika tunawashukuru sana. Tuna imani na Jeshi letu, Mungu awabariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi naomba nitoe maoni yangu kwa ufupi kama ifuatavyo:-

Kwa kuwa hapa Tanzania vijana walioko sekondari na hasa wanaohitimu kidato cha nne, mitihani yao huwa inafanyika mwishoni mwa mwezi wa kumi kila mwaka. Hivyo watoto hawa wanaotajarajia kuendelea na masomo ya kidato cha tano husubiri kwa takribani miezi minane na zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hali hiyo huwa ni kipindi cha mpito mgumu sana kwa wazazi na hata watoto pia kwani mazingira yanaweza kumuathiri mtoto na kujikuta anabadili nia yake ya kuendelea na masomo yake ya kidato cha tano ama wengine kuangukia kwenye tabia za ama kupata mimba au dawa za kulevya au ulevi na tabia nyingine zitakazokwamisha ndoto yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo kutokana na hali hiyo, naomba nishauri kuwa watoto hawa wanaomaliza kidato cha nne, mara baada ya matokeo yao ya mitihani Wizara iandae namna ya kuwachukua watoto hawa kujiunga na JKT kwa miezi kati ya sita na mitatu ili wasipoteze muda bure na pia kutunza uadilifu na nia yao njema ya kuendelea na shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Jeshi la Kujenga Taifa ya mwaka 1964 (na marekebisho yake) kifungu cha 5(2) kinatoa nafasi kwa kijana mwenye umri wa miaka 16 kujiunga na Jeshi hilo; hivyo haitakuwa tatizo kuwachukua wanafunzi hawa. Kwa sheria hiyo Wizara iongee/ishirikiane na Wizara ya Elimu ili kubadili mfumo wa kuwapeleka JKT vijana wanaomaliza kidato cha sita badala yake tunaanza na wanaosubiri kwenda kidato cha tano kwani hawa wana muda wa kutosha sana kuliko wa kidato cha sita wanaosubiri kwenda vyuo vikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, vijana watakaofaulu kuanzia division one hadi division three ndio waweze kupata nafasi ya kujiunga na JKT. Pia itaweza kurahisisha kuwapata wanaotaka kujiunga na Majeshi yetu kama Polisi, Magereza, Uhamiaji, Jeshi la Wananchi na kadhalika kuliko utaratibu wa sasa unaotumika kuwasaka mitaani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho najua jambo hili linaweza kuonekana ni gumu sana, lakini ninaona manufaa yake ni makubwa zaidi, kwani tunaokoa Taifa letu na nguvu kazi pamoja na wasomi na tunapata waadilifu zaidi kwani watoto hawasahau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa naunga mkono hoja asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe pongezi za dhati kwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara hii na watendaji wote. Jambo kubwa la pongezi ni namna ambayo tayari juhudi kubwa za makusudi ambazo zimeanza kuonekana katika suala zima la kutatua tatizo la maji kwa wananchi wa Tanzania. Tumeona miradi mikubwa ikianzishwa. Hata hivyo nina ushauri kwamba hebu Serikali ichukue hatua za makusudi za kuunda tume maalum itakayochanganyika na Wabunge ili waende kwenye maeneo yote ambayo yalidumu kwa muda mrefu bila kukamilika ilhali Serikali inakuwa imetoa fedha za miradi hiyo ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni miaka zaidi ya kumi sasa niko ndani ya Bunge na kila mwaka nimeshuhudia tukipitisha bajeti ya maji hata kama ni kidogo. Je, fedha hizo ni kweli hadi sasa bado hazijatatua angalau kwa asilimia ndogo ya tatizo la maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, kweli inasikitisha kwani zaidi ya fedha za Serikali pia kuna fedha za wahisani zimekuwa zikiletwa nchini. Mimi nina mashaka huenda kuna chungio linapitisha fedha hizi. Hivyo nashauri tume iundwe na iangalie kuanzia miaka kumi iliyopita na fedha ambazo zimeshatoka na kama zilitumika ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni kwa nini Mkoa wa Singida hauna mradi mkubwa wa maji? Naomba na sisi Singida tupate mradi mkubwa wa maji utakaotatua tatizo la maji kwenye mkoa wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuchangia mjadala huu ulioko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Mpango pamoja na timu yako yote, kwa kweli sisi hatuna mashaka na wewe na kadri miaka inavyozidi kwenda naamini mambo yataendelea kuwa mazuri. So, endelea hivyo na Mungu aendelee kukubariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama hapa nataka nichangie ila kwa huzuni sana, nina uchungu sana, kwa sababu alitokea mtoto mmoja akasoma, akalelewa mikononi mwa wazazi wa Chama cha Mapinduzi, akasoma kwa kodi ya Watanzania na wananchi wa Singinda hususani wananchi wa Ikungi Mashariki, Mheshimiwa Tundu Lissu mdogo wangu. Wananchi wa Singida wakamwamini wananchi wa Ikungi Mashariki, wakampa nafasi nenda baba katutetee, ukatuombee shida zetu huku, wananchi wa Ikungi hivi ninavyoongea wanawake wana taabu, walimwamini kijana wao aje alie ndani ya Bunge ili waweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimtegemea kijana wao akawakomboe na shida zao. Naomba niongee kwa ajili ya wananchi wa Ikungi, Ikungi maji salama ni asilimia 25 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara hii leo niwasemee akinamama, naomba maji yaende Ikungi hawana mtetezi humu ndani, kwa sababu mtoto wao kahamia kwa Wazungu. Kwa hiyo, naomba sana maji yaende Ikungi. Hakuna barabara kule, umeme ambao umepelekwa kule ni vijiji 44 tu kati ya… (Makofi/Kicheko)

MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana na mimi kwa kweli naomba nijielekeze kuwatetea wanawake wa Mkoa wa Singida hususani wa Jimbo la Ikungi Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Makyungu iko Singida Mashariki. Hospitali ya Makyungu mpaka sasa hivi huduma za maji pale ni hafifu, naomba sana Wizara kwa sababu Hospitali ile imekuwa ikitoa huduma nzuri sana na kuna ongezeko la watu, naomba Wizara iiangalie kwa jicho la pekee kupeleka maji pale Makyungu ili yaweze kuhudumia wananchi wanaoishi maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumza haya bado nitashukuru sana kwenye Jimbo la Singida Magharibi pale Sepuka, kuna mradi wa maji mkubwa ambao umepelekwa pale, kwa hiyo naishukuru sana Wizara kwa sababu wamepeleka milioni 101, naamini zitasaidia maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeyasema haya kwa sababu nafahamu kazi kubwa ambayo anaifanya Rais wetu, anapaswa kuungwa mkono na watu wanaowatetea wanyonge. Kama kweli wewe ni mtetezi wa wanyonge utapaswa umuunge mkono Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Nasema haya kwa sababu mpaka sasa hivi tunavyoongea akinamama wa Singida hususani Singida Mashariki wanashindwa kwenda kujifungulia kwenye Vituo vya Afya kwa sababu huduma kule hazipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Rais wetu ameamua kulinda rasilimali za Taifa letu ili ziende zikaokoe hata wale akinamama wanaofia njiani kwa sababu ya kushindwa kwenda kwenye vituo vya afya, mtu anasimama anasema amekosea, inauma sana! Nampongeza Rais wangu na tutaendelea kumuombea na nataka kusema hivi, nawapongeza wale wanaompongeza, hata neno la Mungu linasema ni heri uwe baridi au moto kuliko kuwa vuguvugu, kwa sababu ukiwa vuguvugu kinywa cha Bwana kitakutapika, unaelewa maana ninayoisema hii. Ni lazima tumuunge mkono Rais wetu katika juhudi hizi anazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wetu wa Singida, bomba la mafuta linaloenda Tanga, linapita katika Wilaya tatu katika Mkoa wetu wa Singida, wananchi wa Singida wanakwenda kunufaika na juhudi kubwa ambazo zimefanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme hivi, mwizi ni mwizi tu, iwe umeweka mkataba mbovu, usiwe mbovu, mwizi ni mwizi na akikamatwa achukuliwe hatua. Nilimsikiliza Rais wetu, ameonesha huruma kubwa sana amesema jamani njooni tuzungumze ili mtulipe pale mlipoona mmetuibia tatizo liko wapi? Naomba tumpongeze Rais wetu ili hawa watu ambao naamini kesho na kesho kutwa tutawaona wanaenda kutaka suluhu kwa ajili ya kutulipa, kwa hiyo nataka nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine pale Londoni na pale Sambaru huko Mashariki ya Singida, kuna matatizo makubwa ya wachimbaji wadogo, nategemea tusimame kuweza kuwatetea wachimbaji wadogo pale, tukimuunga mkono Rais wetu, hata wachimbaji wetu wadogo pale watanufaika na mradi uliopo pale. Mwekezaji aliyepo pale tangu 2006 mpaka sasa hajalipa compensation, mpaka sasa wananchi wanahangaika, naomba sana tumuunge mkono Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kengele ya kwanza, kabla sijamalizia nataka nimalizie kwa kusema hivi, Mheshimiwa Magufuli songo mbele, ukiona watu wanakupinga, ujue kuna jambo limejificha nyuma yao, ama wanaona aibu na upinzani wa kupinga kila kitu utajipinga hata wewe mwenyewe, kuna mambo ambayo utayasema leo kwa sababu ya kupinga, utapinga kesho. Mheshimiwa Rais wetu naomba usonge mbele, wanaokupinga ni kwa sababu wanaona nchi hii inakwenda kupaa, nchi hii inakwenda kunufaika na kwa sababu wanapinga na ni wachache wala hawatuwezi humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimalizie kwa kusema hivi, ngoja nikae sawa…..

(Hapa Mheshimiwa Mbunge aliimba -Kanyanga twende Magufuli wetu, Kanyaga twende, usiogopeeee)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pia naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi jioni hii ya leo ili na nitoe mawili, matatu kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Manaibu wake na Watendaji wengine kwa kazi nzuri wanayoifanya, lakini bado naomba niendelee kumtia moyo sana Rais wetu nimefarijika sana kwa michango ambayo imeendelea kutoka kwa upande wa pili kwa sababu nimeona hakika msumari kwa kweli umeingia na ndiyo maana maneno ya kupinga kila kitu ambacho ni kizuri yameendelea kutoka ndani ya nyumba hii, hivyo naomba kuendelea kumtia moyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze mawili, matatu. Kwanza nipongeze sana kwenye mpango uliopo katika kitabu hiki hasa kwa upande wa Mkoa wangu wa Singida, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri. Nianze na upande wa Daraja la Sibiti pamoja na barabara aliyoitaja kutoka Mbulu kuja Haydom hadi Sibiti kwenda Maswa. Fedha alizotenga kwa kweli ni ndogo sana sielewi hizo fedha ni za nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana barabara hiyo ya Sibiti pamoja na kwamba inaenda Mbulu, naomba itoke Sibiti ije Mkalama ije Nduguti ije hadi Iguguno iwe ya lami. Hatuwezi kujenga daraja zuri lenye kiwango kikubwa lakini barabara isiwe ya lami, naomba sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona Mheshimiwa Waziri ametaja daraja la Msingi, naomba sana daraja lile kuna madaraja mengine madogo madogo ambayo naamini TARURA itaenda kuyafanyia kazi, lakini naomba sana barabara ile ambayo imepita Kinampanda kushuka Msingi kwenda Gumanga imaliziwe iwe ya lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia barabara ya kutoka Singida Mjini kupita Sipuka hadi Ndago kwenda Kizaga. Ile barabara ni ya lami na ni ya ahadi ya Rais, naomba sana sijaona kama Mheshimiwa Waziri ameitaja, nashukuru kwa zile ambazo amezitaja, mimi nataja zile ambazo bado hajazitaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishukuru kwa kipekee naomba Mheshimiwa Waziri apeleke salamu kwa Mheshimiwa Rais, barabara inayotoka Tanga inayopita Kondoa inakuja kwa Mtoro inakuja Simiyu hadi Singida barabara ile ni kwa ajili ya Bomba la Mafuta ambalo litakuja kuinua uchumi mkubwa sana kwa wananchi wa Singida. Napongeza sana na nashukuru lakini fedha walizotenga hazitutii moyo sana, naomba atakapokuja atutie moyo kwamba zitamalizika lini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kuwapongeza watu wa mawasiliano. Nawapongeza TTCL kuna mmoja alizungumza kwamba Watanzania sasa tujivunie shirika letu, ni kweli na naunga mkono. Naomba sana TTCL wapewe uwezo mkubwa wa kutandaza mtandao nchi nzima ili wananchi walioko vijijini waweze kupata mawasiliano ya kutosha, lakini naomba hasa kwenye maeneo ambayo ni hatarishi kwa mfano Sekenke pale ukiwa unashuka ule mlima Sekenke hamna network, mtu akipata tatizo hawezi kuwasiliana. TTCL naamini wameshakuja vizuri wana-perform vizuri, wawezeshwe ili waweze kuweka mtandao nchi nzima wananchi waweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TBA wamefanya kazi nzuri, naomba waongezewe bajeti ili waweze kukarabati na yale majengo ambayo yamechakaa sasa hivi. Kwa mfano ya hapa Dodoma wanayoishi Waheshimiwa Wabunge, yamechakaa waongezewe ili waweze kukarabati yale majengo. Wapeni nafasi waweze kujenga hapa Dodoma majengo ya Serikali kwa sababu majengo yao nikiyatazama ni yanadumu na ni imara, yanaishi kwa muda mrefu. Wawezeshwe ili waweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, naomba sana kwenye upande wa barabara za vijijini kuna TARURA, TANROAD Mkoa na kuna Taifa. Mheshimiwa Waziri atakapokuja naomba aje atufafanulie vizuri barabara zipi hasa maana yake zile tunazozitaja, kwa mfano ukienda Singida kuna yale madaraja makubwa ambayo atasema hizo barabara ni za vijijini, lakini TARURA hataweza kwa sababu ya bajeti ndogo. Kwa hiyo, naomba sana watakapokuja hapa waje watufafanulie TARURA… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nashukuru kwa kupata nafasi hii ili niweze kuchangia hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na pongezi. Pongezi hizi nazipeleka kwa Mheshimiwa Rais kwa kauli yake ya kuhakikisha kwamba elimu bure kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne. Tumeona mafanikio makubwa ya watoto ambao walikuwa wamekaa majumbani wanashindwa kwenda kuandikishwa kwa sababu ya fedha ambazo zilikuwa zinatakiwa shuleni. Baada ya tangazo la elimu bure sote tumeshuhudia mafuriko ya watoto waliokwenda kujiandikisha. Wapo wanaobeza kaulimbiu hii ya elimu bure wakifananisha na kwamba Serikali haikujiandaa, lakini nataka kupongeza kwa sababu Mheshimiwa wewe ulikuwepo tulipoanzisha shule za sekondari za kata, angalia sasa hivi ukienda kwenye vyuo vikuu vyetu watoto wa shule za sekondari za kata ndiyo waliojaza vyuo vikuu vyetu hapa nchini, hayo ni mafanikio makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili uweze kufanikiwa ni lazima uamue na uthubutu ili uanze. Changamoto zinazojitokeza ndiyo mafanikio yenyewe. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba nikupe moyo, kazi ni nzuri, tuendelee, tuwachukue watoto wote, asiachwe mtu nyuma eti kwa kisingizo kwamba elimu bure inawajaza watoto bila huduma kwa sababu Serikali haikujiandaa. Serikali mmejiandaa na wananchi wamejiandaa, nimeshuhudia kwenye Mkoa wangu wa Singida, nipende kuwapongeza Wabunge wote wa Majimbo ya Mkoa wa Singida wamejitahidi sana na Madiwani wote wa Mkoa wa Singida wameweza kusimamia ujenzi wa kuongeza madarasa ya wanafunzi hawa walioongezeka na watoto wako madarasani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi upande wa shule za kata nimeshapongeza na watoto sasa hivi wako vyuoni wanaendelea na masomo isipokuwa naomba niishauri Serikali kuanzishwa kwa shule maalum kwa ajili ya masomo ya sayansi. Hatuwezi tukazifanya shule zote zikawa na masomo ya sayansi kutokana na upungufu wa walimu tulionao. Kwa hiyo, cha msingi ni kuanzisha shule maalum ili walimu wale wapelekwe kwenye hizo shule ambazo tutakuwa tumezianzisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka nizungumzie suala la mikopo ya elimu ya juu. Mheshimiwa Waziri amezungumzia ni namna gani wanafunzi ambao wamebainika ni wadaiwa sugu takribani 147,000 na ukasema 42,000 ndiyo wameonesha nia ya kutaka kuchangia, sasa mimi naomba niulize, hawa wengine 103,000 au 100,000 wako wapi? Je, wana ajira ya kuweza kulipa? Kama hawana Serikali inaweka mkakati gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali kwamba wanafunzi wetu hawa tunaowakopesha wanapomaliza elimu ya juu tujitahidi wapate ajira, tuwasaidie ili waweze kurudisha mikopo yetu kwa sababu wakibaki mitaani watashindwa kurudisha mikopo yetu. Pamoja na kwamba watatakiwa wakidhi vigezo, lakini bado wanafunzi hawa watambulike hata kwenye Halmashauri zetu kwa sababu kuna mikakati ya ule Mfuko wa Vijana, Wanawake na Walemavu wanaweza wakawezeshwa kwa sababu tunasema uchumi wa viwanda, wawezeshwe waweze kujiajiri wenyewe, Serikali iwafuatilie, isiwaache hivi hivi, iwasaidie ama waajiriwe ama waweze kujiajiri wenyewe.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo nilisimama siku moja hapa nikaomba mwongozo kwamba wanafunzi wanapo-qualify kupata mkopo iwe ni nusu au asilimia 100 cha kushangaza wanapofika vyuoni wanasumbuliwa sana. Inatakiwa walipe wanasema advance payment ambayo inawasumbua sana watoto wetu. Kumbuka watoto wengi wanaotaka mikopo ni watoto wa wakulima wetu, waliosoma shule hizi za kata, baba auze nyanya, mahindi au asubiri auze alizeti kwa mfano kule Singida au vitunguu, unakuta zile fedha hazitoshi, anapofika kule anateseka.

Mimi nina watoto ambao walifika mpaka vyuoni leo hii wamerudi kwa sababu walishindwa kulipa ile advance payment ya shilingi 600,000. Naomba jambo hili Mheshimiwa Waziri utakaposimama hapo utufafanulie umelichukuliaje na Serikali inasemaje ili tuwanusuru watoto wetu hawa ambao wanakwenda kuteseka, itawakatisha tamaa wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli naomba nimpongeze sana Profesa Kikula, mimi nilikuwa Mjumbe wa Kamati ya Huduma za Jamii, wakati tunakwenda kukagua maeneo ya kaunzishwa ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma, tulipofika kule kwanza magari yetu yalikuwa hayawezi hata kupita wakati tunaukagua ule mlima, tukasema hivi ni nani atakayekabidhiwa kuja kusimamia chuo hiki ili kitambulike na kiwe chuo bora? Tunamshukuru Rais wa Awamu ya Nne alimteua Profesa Kikula, wakatafuta pesa, Serikali ikakijenga kile chuo ambacho sasa hivi tunajivunia kwamba ni chuo kikuu ambacho kinachukua wanafunzi wengi sana.

Mheshimiwa Waziri mimi sifahamu wewe kwenye Wizara yako, huyu Profesa angepata award kwa sababu aliweza kusimamia vizuri sana pamoja na changamoto zote ambazo zilikuwa zinajitokeza pale, amesimamia vizuri sana. Hakuna ubadhirifu wa pesa, kwa hiyo, mimi kwa kweli nimeona leo nimpongeze Profesa Kikula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kwenye upande wa shule za kata bado kuna changamoto kubwa sana kwa watoto wetu wa kike. Watoto wetu wa kike wanakaa mbali, wanapopangiwa kwenye zile shule wanakwenda kupanga kwenye nyumba za watu wanapata changamoto kubwa sana ya masomo. Wengine wanashindwa kuendelea na masomo kwa sababu wanakatishwa tamaa, miluzi ni mingi sana kwa watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali hii ianze kumjali mtoto wa kike, zijengwe hostel kwa ajili ya kumhifadhi mtoto wa kike. Sikatai kwamba na mtoto wa kiume anapaswa alindwe, lakini bado kwa mtoto wa kike hali ni ngumu sana, anasoma kwenye mazingira magumu sana. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuomba sana uangalie suala la hostel za watoto wa kike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kuna suala la vyoo mashuleni. Tumegundua watoto wa kike wamekuwa wakiadhirika sana kwa sababu shule nyingi bado hazina vyoo vya kutosha na fedha ziko kwako siyo TAMISEMI. Kwa hiyo, naomba sana fedha zitolewe kwenye shule kwa wingi kwa ajili ya kujenga hivi vyoo lakini ramani ile ya vyoo lazima iwe na choo kinachoweza kumsitiri mtoto wa kike anapokuwa kwenye siku za maumbile ya mtoto wa kike ili aweze kusitirika kwa sababu walio wengi wanakata tamaa hata kwenda shuleni. Akishapitwa ile wiki moja anapokuja wiki ya pili kwa kweli anakuwa amenyong’onyea sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishie hapa, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, aluta continua, tuko pamoja Mheshimiwa Rais, kaza buti, tafuta pesa, tunajua unatafuta pesa ili shule zetu ziweze kuwa za standard, tupate walimu wa kutosha lakini zile shule pia hebu zipekelewe visima vya maji ili kuwe na maji ya kutosha kwenye shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru. Ninaamini nina dakika kumi.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuona umuhimu mkubwa sana katika sekta ya uvuvi pamoja na mifugo, ndiyo maana ameiweka Wizara hii ili tuweze kupata nafasi kubwa sana katika kujadili changamoto zote zinazogusa sekta hii. Kwa hiyo ninampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaamini kabisa kwamba pasipokuwa na changamoto, hakuna mafanikio. Kwa hiyo, ninaamini kwa changamoto zote zinazojitokeza katika sekta ya uvuvi pamoja na mifugo ndiko tunakoelekea kwenye mafanikio. Ninaomba sana Wizara ipokee changamoto hizo na izifanyie kazi kwa sababu ndiyo hasa ilikuwa kusudio la Mheshimiwa Rais ili kuweza kuwasaidia wale wananchi ambao wanaguswa na sekta hii.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wangu wa Singida tuna ufugaji. Kwanza ni wafugaji lakini pia wakulima, tumekuwa na ufugaji mzuri na ukulima bila migogoro kwa muda mrefu sana. Migogoro huwa inakuja pale wageni wanapokuja kuingiza mifugo kwenye maeneo ambayo wenyewe hatukuwa tumekusudia kwa ajili ya kulisha mifugo lakini Serikali za Mkoa, Vijiji na Wilaya wemekuwa wakijadili na kuingia muafaka.

Mheshimimiwa Spika, kuna jambo ambalo Mheshimiwa Waziri katika taarifa yako, sielewi kama kweli unaona ufugaji wa kuku ambao hasa uko katika Mkoa wa Singida ni sehemu mojawapo ya kuwaondolea umaskini Watanzania, pia ni kipato kinachotokana na ufugaji wa kuku, sijaona kama umetilia mkazo. Singida kuku ni chanzo cha kipato, lakini bado ni chakula na ni utamaduni wetu. Hata mtoto mdogo ukienda kumtembelea shangazi, anakupatia kuku kwa ajili ya kwenda kumfuga, kumuendeleza. Ni utamaduni wetu mgeni akifika ni lazima kwanza mboga ya haraka ni kuku. Waziri unatakiwa sasa uwatoe wananchi wa Mkoa wa Singida kwenye utamaduni kwamba ni ukarimu tu, iwe ni biashara tena biashara yenye tija kwa wananchi wa Mkoa wa Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wataalam walioko kule uwape maelekezo kama ambavyo mnaweza kutoa maelekezo kwenye mazao mengine, pia kwenye ufugaji wa kuku utoe maelekezo wataalam waende wakawasaidie na kutoa dawa, wafuatiliwe ili kuweza kukuza ufugaji wa kuku wa Singida ambao ni watamu sana wote mnafahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikitoka kwenye eneo hilo niende kwenye uvuvi. Na sisi pia tuna uvuvi Singida, ukienda Ziwa Singidani na Kindai. Pia nataka nizungumzie Kitangiri. Kwanza nataka ieleweke na Waziri utakaposimama hapo useme, Wilaya ya Iramba ndiyo yenye Ziwa Kitangiri, useme hapa leo ili wananchi wote wasikie, kwa sababu Kitangiri tunaita Kiteka, wavuvi wanaovua pale wanaotoka upande wa Meatu, kwanza Serikali ya Halmashauri ya Meatu haitendei haki Serikali ya Halmashauri ya Iramba.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Iramba inapofunga ziwa lile kwa ajili ya kuhakikisha vifaranga wale wanakua, Meatu hawafungi na wakati haiko kwao! Ushuru wanapokea wao, hela zile haziji Iramba, kwa hiyo tunawadhulumu na hatuwatendei haki wananchi wa Iramba na Meatu wanakaribisha watu kutoka maeneo mengine. Wanapokea ushuru, unanufaisha Halmashauri ya Meatu. Sawa, sikatai lakini ninaomba taratibu zifuatwe. Iramba inaposema tunafunga ziwa hili, Meatu pia watangaze, wafunge! Pia ninaomba sana boti iletwe kwa ajili ya kufuatilia wale wavuvi haramu ambao hawana leseni na vibali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna mkondo wa maji ambao umekuwa ukipitisha maji kwenda Kitangiri. Kata za Igunga wamekuwa wakilima kwenye mkondo ule kiasi kwamba inatishia Kitangiri kuondoka. Mheshimiwa Waziri naomba utakapoongea hapo utuambie unatulindia vipi Kiteka yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikimaliza Mkoa wa Singida mimi naomba niseme hivi, kuna suala la operation linaloendelea. Mheshimiwa Mpina una baba zako, una wadogo zako, una kaka zako, wote wako kwenye uvuvi, hata kama hujazaliwa nao kumbuka kila mtoto au kila mwanaume au kila mwanamke ni mtoto wa mwanamke aliyezaliwa na wanawake kama sisi. Ni hakika wale wavuvi hawatendewi haki. Mnapokamata zile nyavu unazichoma, kumbuka ameacha familia nyuma inamtegemea, kumbuka ana wazazi wake wanamtegemea, kwa nini usiende na utaratibu mzuri? Nyang’anya zile nyavu lakini lete mbadala wape nyavu nyingine, hata kama watalipia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kwa kweli siungi mkono hiyo operation ni uchungu kwa sababu na mimi nina ndugu zangu wako kule. Kwa hiyo, naomba mnapochoma yale sijui makokoro, sijui kitu gani, naomba peleka nyavu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ameongea hapa Mbunge mmoja kwamba wasomi mliopo huko msifanye kazi kama watu ambao hamkwenda shule. Mheshimiwa Rais amewaweka hapo ili muwasaidie Watanzania na ili msaidie sekta hiyo. Kwa kweli hatuungi mkono uvuvi haramu, lakini ile operation namna mnavyoiendesha kwa kweli haitendi haki kama binadamu wengine. Kwa hiyo, suala hilo naomba sana liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna jambo lingine hili la kuwabandika ng’ombe moto. Jamani, chuma cha moto kwenda kumbandua ng’ombe na kumfanya awe na kidonda. Mimi nimekutana na ng’ombe ana kidonda hakiponi. Naomba mtafute namna ya kuweka chapa wale ng’ombe. Jamani, kwanza tunaharibu ile ngozi halafu ng’ombe anakonda. Naomba sana Mheshimiwa Mpina, wataalam wapo na mmesoma kwa kweli, tafuteni namna ya kutia chapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli, tunajua tunataka tudhibiti ng’ombe wanaotoka katika nchi jirani, lakini kwani mtu akisajili ng’ombe wake akasema Mheshimiwa Mlata ana ng’ombe 100, kesho mkimkuta ana ng’ombe 200 si atajieleza kawapata wapi? Tafuteni namna, basi wawekeeni hata vidani, wawekeeni kitu chochote wale ng’ombe jamani, tusiwatese jamani. Kwa hiyo, hilo mimi nilikuwa naomba liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, sisi tulikuwa tunapokea ng’ombe kutoka Meatu, Maswa, wanakuja pale Singida kupakia. Mabehewa yalikuwa yanapakia kupitia hii reli ya hapa Manyoni, lakini siku hizi usafirishaji wa ng’ombe umekuwa ni mgumu kwa sababu ile treni haiendi tena. Sasa sifahamu mna mawasiliano gani na sekta ya uchukuzi ili kuwapunguzia ng’ombe msafara mrefu, wengine wanafia njiani kwa sababu ile reli ilikuwa inarahisisha sana yale mabehewa kupakia ng’ombe wengi lakini na sisi Singida tulikuwa tunaweza kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, boresheni ranchi zenu, ukienda Kongwa kwa Mheshimiwa Spika, yale majani yanaota mpaka yanakauka, hakuna chochote kinachopatikana. Wekeni utaratibu mtu akiingiza ng’ombe mmoja mwambie kiasi fulani, mtu alete ng’ombe wake, alishe, kusanya hela, muwekee maji pale, alipie kama kuna matibabu, hebu fanyeni biashara kisomi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ya kutoa mchango wangu kwa njia ya maandishi katika Wizara hii. Naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri sana wanayoifanya. Nampongeza Katibu Mkuu na Naibu wake na watendaji wote na Wakuu mbalimbali wa Idara zote zilizoko Wizarani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze sana na kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa dhamira yake ya dhati ya kutaka kuinua Taifa letu katika Diplomasia ya Uchumi na uhusiano mzuri na Mataifa mengine duniani kwa kuwapa nafasi wataalam wake kufanya kazi hiyo bila yeye kukanyaga katika nchi hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakika uamuzi wake wa kuwaamini na kuwapa nafasi wataalam wote wakiwepo Mabalozi wetu wote walioko nje ya nchi na waliopo ndani ya nchi. Uwezo wao wa uzalendo wao, tumeuona kwani mahusiano ya Taifa letu yamezidi kuwa mazuri na kuimarika, kiuchumi, kiusalama na kisiasa, ahsante sana Mheshimiwa Rais na hongera sana watendaji na Mabalozi wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kazi kubwa sana inayofanywa na Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu ya kumwakilisha Mheshimiwa Rais kwenye mikutano mbalimbali na majukumu mbalimbali ya Kimataifa, huko nako hatujapungukiwa. Pia pongezi kwa Mabalozi ambao wao wako hapa Tanzania, lakini nchi nyingine ya kuibua mazuri yote kwenye Kanda wanazozisimamia mfano, Mabalozi wanaosimamia Idara mbalimbali kama; Mashirika ya Kimataifa, Kanda ya Afrika, Kanda ya Asia, Kanda ya Ulaya na Kanda ya Amerika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza sana hawa balozi wanaosimamia Kanda hizi. Kwani mambo yanaenda vizuri sana tumeona viongozi mbalimbali wakija nchini na wafanya biashara wengi wakija nchini kwetu, pongezi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nipongeze utaratibu nzuri sana ambao Wizara imefanya wa kuleta vitabu ambavyo vina anwani za Balozi zote zilizoko nje ya nchi na ndani ya nchi yetu, pongezi sana. Pia kitabu kizuri cha utekelezaji wa diplomasia ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda 2020. Utaratibu huu ni mzuri sana, naomba uendelee na ikiwezekana, angalau kuonyeshwe na moja ya fursa iliyoko katika nchi husika. Pongezi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa ushauri kuhusu nyumba na majengo ya baadhi ya Balozi zetu nje. Majengo haya yanatia doa nchi yetu kwa uchakavu. Naomba Waziri alipeleke shauri hili kwenye Baraza la Mawaziri ili jambo la bajeti ya kukarabati nyumba hizi lichukuliwe na Hazina, Wizara haitaweza bajeti yake ni ndogo. Mfano, nyumba za London niliwahi kwenda, haziridhishi. Naomba sana u-smart wa mtu humpa heshima kwa wanaomtazama. Hivyo, tunaweza tukadharaulika na Mataifa mengine kutokana tu na uchakavu wa majengo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na utaratibu wa kubadilishana wafungwa, Je. Serikali inasemaje juu ya kuwarejesha Watanzania ambao wamehukumiwa kwa makosa mbalimbali duniani?

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hizi mbili. Kwanza niwapongeze Mawaziri wote Mheshimiwa Selemani Jafo pamoja na Mheshimiwa George Mkuchika, Naibu Mawaziri George Kakunda na Josephat Kandege, Makatibu Wakuu wote katika Wizara hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi nimpongeze sana Mheshimiwa Jafo na Manaibu wake kwa kazi kubwa ambayo tumeiona. Wamekuwa wakitembelea Halmashauri zetu na maeneo yetu yote kuhakikisha kwamba shughuli za maendeleo zinamfikia mnyonge kama Rais wetu ambavyo amekusudia. Nampongeza sana Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Selemani Jafo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami niungane na wale wote wapenda maendeleo waliompongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. Naomba apelekewe salamu na akubali kwamba yeye kuwa mti ule uzaao matunda yaliyo bora na yaliyo masafi na yaliyo mazuri, kwa sababu mti wa namna hiyo ni lazima upigwe mawe ni lazima upigwe vijiti na ni lazima unenewe maneno yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba akubali kwamba yeye ni mti uzaao matunda yaliyo mema na ndiyo maana wale wasiopenda mema wanamrushia mawe. Naomba pia apelekewe salamu kwamba wananchi wa Mkoa wa Singida tuko pamoja na yeye, tunamuunga mkono kwa kazi kubwa na nzuri ambayo ameendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyoongea upande wa miundombinu barabara za Mkoa wa Singida nyingi zinapitika hata kama ni za vumbi kwa sababu wale akinamama walioko pembezoni hata wanapotaka kupata huduma za afya kuna bajaji, kuna bodaboda, kuna Noah. Wakifika hospitali wanakuta nidhamu ya watumishi iko safi, dawa ziko nyingi, Rais ameongeza bajeti kubwa, vitendea kazi vipo, wafanyakazi wanafanya kazi nzuri ya kuwahudumia wananchi. Tunamuunga mkono aendelee tuko pamoja naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho nasikitika sana mpelekeeni salamu Mheshimiwa Rais mwambieni atusaide tupate upinzani utakaosaidia kujenga Taifa hili, Upinzani unaojitambua, Upinzani unaojitambua, Upinzani ulio bora, Msajili wa Vyama awapeleke Wapinzani kwenye nchi zenye Upinzani wenye mfano ambao Mataifa yao yameweza kusimama imara. Nasema hivi kwa sababu hapa Tanzania bado hatujawa na Upinzani ulio imara, Upinzani utakaosaidia katika Taifa hili ili tuwasaidie wanyonge na kulijenga Taifa letu. Mpelekeeni salamu kwamba, bado hatuna Wapinzani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Rais...

T A A R I F A . . .

MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei taarifa hii kwa sababu Upinzani uko wapi wa kuruhusiwa kwenda kufanya mikutano kwa wananchi, Upinzani unaoenda kuwahadaa wananchi wasifanye shughuli za maendeleo, wakae wanaandamana barabarani, Upinzani unaomkataa Rais, Upinzani usioona yale mazuri, Upinzani ni upi utakaoruhusiwa kwenda barabarani.

T A A R I F A . . .

MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, iwe Vyama vya Mageuzi, iwe ni Upinzani lakini mimi nasema Upinzani gani hata mambo mazuri wanayakataa? Rais amejitoa kwa ajili ya Taifa hili...

KUHUSU UTARATIBU . . .

MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nilikuwa kwenye utawala bora lakini sasa nataka kusema mwambieni Rais kwamba yale yote anayoyafanya wako watu watakuja kuyakumbuka kama ambavyo wanamkumbuka Jakaya sasa hivi, asonge mbele aendelee kuwa mti uzaao matunda mema, watakuja kumkumbuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizo ambazo nampa Mheshimiwa Rais, tunamshukuru sana Mheshimiwa Selemani Jafo kwa sababu katika Mkoa wetu wa Singida ametuletea hospitali mbili, hospitali ya Mkalama pamoja na Ilongero. Naomba hospitali hizo zikajengwe mahali ambapo amezipanga. Pia naomba sana hospitali ya Ilongero itakapokwenda kujengwa pawe ni pale ambapo ndipo maeneo ya Makao Makuu ya Halmashauri ile, hivyo naomba Mkurugenzi ahamie haraka eneo lile ambalo mwaka 2006 ndiyo tulipitisha kwamba patakuwa ni Makao Makuu. Namwamini na naomba atembelee eneo lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana nizungumzie suala la afya. Naomba kuuliza, Mheshimiwa Rais ametoa fedha nyingi sana kwa ajili ya dawa zile Delivery Kits kwa ajili ya kujifungua vile vitu ni vya bure kwa nini wanauza au ni ule mfuko ndiyo wanataka kuuza? Watoe ule mfuko waache vifaa waweke labor, wanawake wapate vifaa bure, wasiuze ile kits au set kwa ajili ya wanawake. Kumbukeni pia kujenga mama ngojea kwa ajili ya kuokoa akinamama wenye matatizo ya uzazi ili waje wasubirie pale, hilo naomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, naomba sana hebu tuangalie Kata ya Mwanga kule Mkalama, hata nguzo moja ya umeme haijawahi kupelekwa, kwa sababu tunataka kujenga uchumi wa viwanda na kule ndiko kwenye kilimo cha vitunguu, alizeti na mahindi, tunaomba wapeleke nguzo na hatimaye waweke umeme kule. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyoniona haya ndiyo madini yetu tunayoenda kuyajadili leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mchango katika Wizara hii ya Madini ambayo ni muhimu sana kwa Taifa letu na wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwanza kabisa kwa kuona umuhimu wa Wizara hii na kuitenganisha kutoka kwenye nishati ikabaki kama Wizara ya Madini. Aliona umuhimu na kweli Wizara hii ina mambo mengi makubwa ambayo yanastahili kuwa na Wizara peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze kwa kuweza kumteuwa Waziri, mdogo wangu Mheshimiwa Angellah Kairuki kwa sababu nina imani naye. Kwanza ni mwanasheria, lakini ni mzalendo. Wizara hii inatakiwa mtu mzalendo kama alivyo Waziri, Naibu Mawaziri Mheshimiwa Doto Biteko shemeji yangu na mwanangu Mheshimiwa Stanslaus Nyongo. Naamini kabisa mtaitendea haki Wizara hii ili tuweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kuonesha uzalendo namba moja. Mheshimiwa Rais kabla hajawa Rais alionesha uchungu wa namna gani nchi yetu ilivyokuwa inafilisiwa, madini yalikuwa yanapelekwa nje kwa kisingizio cha mchanga, sijui makinikia, akajitoa mhanga ili kuweza kulinusuru Taifa letu kwenye sekta hii ya madini. Nampongeza sana. Najua aligusa mahali ambapo watu hawakutegemea kuguswa. Ndiyo maana bado kuna vibaraka wanazungumza kutetea yale yaliyokuwa yakinyonya Taifa letu, namtia Mheshimiwa Rais moyo, songa mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Nabu Spika, niliwahi kusema humu ndani, ndiyo maana Mungu aliamua ajitenge mbali na sisi asionekane kwa sababu angeonekana hakika tungemsumbua. Ikiwa ni jua tutamwambia jua linawaka, ikiwa ni mvua tutasema hii mvua ya nini, ikiwa ni kimbunga tutasema kimbunga cha nini, ikiwa ni utulivu tutasema hewa hamna. Ndiyo mwanadamu alivyo, hasa wengine ambao wanaonesha tabia zao hapa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza kwa kujenga ukuta kwa sababu amelinda mali ambayo tumeona hata kwenye vyombo vya habari watu wanajimilikisha tanzanite ambayo siyo ya kwao. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa hatua ya kujenga ukuta pale Mererani. Hata kama tungejenga kama Mnara wa Babeli ili mradi tunalinda mali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipongeze pia Tume ambayo ameiunda sasa hivi. Naomba Tume hii iliyoundwa inisikilize kwa makini, kwanza ikafanye kazi, lakini kuna sheria ambayo inasema first come first served. Naomba sheria hii ikaangaliwe tena kwa sababu haiwezekani
tukatumia online tukawa tunauza madini yetu online, unamuuzia mtu ambaye humjui. Mheshimiwa Waziri naomba ulisimamie jambo hili ili GST, kwanza nawapongeza kwa vitabu hivi ambavyo wamevitoa, wameonesha kila mkoa na madini yake kila mahali, japokuwa naamini hawajamaliza kwa sababu madini bado ni mengi. Wawezeshwe waende wakafanye utafiti ndipo tuweze kuuza vitalu hivyo baada ya kujua ardhi hii ina mali gani. Tusiwe tunauza tu unampa mtu yeye eti ndiyo aje akwambie hapa kuna madini kiasi fulani, ndiyo maana tunaibiwa. Tuhakikishe kwamba kwanza hiki kitalu kina madini kiasi gani halafu tuweke mnada. Kwa sababu nchi nyingine wanafanya hata mnada, kwa nini tusifanye mnada wa vitalu vyetu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashauri badala ya kumpa mtu akatafiti mwenyewe, tutafiti wenyewe halafu ndiyo tufanye mnada. Tuende tukaone nchi nyingine walivyofanya ili tuweze kupata mapato yatakayokidhi kile kilichopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wananchi wanaoishi kwenye eneo lile jamani, pamoja na kwamba ni mali ya Serikali, lakini wananchi wa eneo lile wafanane basi na madini hayo yaliyopo pale. Kuwe na utaratibu wa kuweza kuwasaidia waondokane na ule umaskini wafanane na madini yanayopatikana pale na huduma ziwekwe pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri suala la One Stop Centre, kwani suala la Madini House limeishia wapi? Madini House siyo ofisi ya kukaa watu, ni wachimbaji wadogo wapate mahali pa kwenda kuuza madini yao na Serikali mnaweza mkanunua, mkaweka mashine ambazo zitatambua madini yaliyo halali na halisi, inaweza ikasaidia kukuza pato au shilingi yetu ikapanda. Kwa hiyo, naomba tuwe na sehemu moja ya wachimbaji wetu ili waondokane na kulaghaiwa na wale wanunuzi wadogowadogo na pia Tume iweke bei elekezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kwenye shamba kuna mabwana shamba, kuna mabwana nyuki, sijui bwana kilimo, sijui bwana samaki, kwa nini kwenye madini kusiwe na mabwana madini? Hawa wawe washauri wa wachimbaji wetu wadogo ili wao wawe ni washauri tu na watoa leseni wawe watoa leseni. Tumeshuhudia wachimbaji wadogo wanapogundua madini anamuendea mtoa leseni, badala ya kumsaidia anauza kwa mtu mwingine eneo lile lakini kukiwa na bwana madini, bwana madini atatoa ushauri tu ili afuate taratibu za kuweza kupata leseni. Mheshimiwa Waziri naomba sana mabwana madini, kama ilivyo bwana nyama, bwana shamba, bwana kilimo, bwana nyuki na mambo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuwe na bei elekezi. Mbona kwenye kahawa kuna bei elekezi, kwenye korosho kuna bei elekezi na mazao mengine kwa nini hakuna bei elekezi kwenye madini? Kwa hiyo, naomba sana suala hili la bei elekezi nalo liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, Singida tuna madini yanaitwa zircon , Iramba, niliwahi kuuliza ile zircon imeambatana na almasi lakini wanunuzi wananunua kama zircon, wanawadhulumu wale wachimbaji. Bado naitaka GST wafanye utafiti watuambie hiyo ni zircon peke yake au ni pamoja na almasi na wafanyeje? Maana hata Tume ya makinikia iliwahi kuzungumza jambo hilo. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri jambo hilo liweze kushughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, wachimbaji wadogo hebu na wao wawe wanaangaliwa kwa sababu wao ndiyo wanakuwa wamegundua lile eneo, lakini anakuja mtu mwingine mnawaambia kwamba hili eneo lilikuwa la utafiti, lakini aliyegundua ni mtu mwingine, matokeo yake mnakuja kutoa leseni kwa watu wengine. Naomba Waziri kwa sababu namwamini sana, naamini atasimamia jambo hilo ili wachimbaji wetu waweze kupata haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante sana.
The Written Laws (Miscellaneous Amendment) (No.2) Bill, 2016
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nami pia naomba niungane na wasemaji waliotangulia, lakini nampongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kututeulia ma-DC ambao tunaamini watakuja kuungana na kaulimbiu ya Hapa ni Kazi Tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana jirani yangu hapa kwenye kijiji chetu cha Maisha Plus, kwa sababu katika kiti hiki alipoteuliwa Mheshimiwa Lucy Mahenga kuwa DC, nilimpongeza na katika kiti hiki pia naomba nimpongeze kwa kustaafu na nimshukuru sana kwamba alikuwa ni DC mzuri katika Wilaya yetu ya Iramba. Hakika tutamkumbuka na tutakumbuka yale mazuri yote aliyotufanyia. Nawapongeza ma-DC wengine kutoka Mkoa wa Singida, waliostaafu na wengine ambao wamepangiwa vituo vingine, basi nawatakia kheri huko kwenye majukumu yao mengine mapya.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nami pia naungana na wenzangu kumpongeza Mwanasheria Mkuu na Waziri wa Katiba na Sheria kwa kutuletea marekebisho haya. Niende moja kwa moja kwenye sheria ya elimu. Kifungu cha 60 (a) ambacho kinatamka wahusika wa adhabu husika kwamba anayesaidia, anayeshawishi na anayeacha mwanafunzi wa Shule ya Msingi au Sekondari kuoa au kuolewa watapata adhabu hiyo ambayo imeainishwa hapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, bado napata mashaka kidogo kwenye kipengele hicho labda Mwanasheria Mkuu tusaidie ili uongezee. Je, anayesaidia ambaye anashindwa kutoa ushirikiano wa kumpata hasa ninamtaja huyu mtoto wa kike; mtoto wa kike anaweza akapewa mimba halafu asimtaje aliyempa mimba ama kwa sababu ametishiwa ama kwa sababu amedanganywa kwamba mwenzako akifungwa utakosa mtu wa kukutunza. Kwa hiyo, mtoto yule anakaa kimya, hataki kutoa ushirikiano.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba sheria itamke, ni nini hasa ili huyu mtu aweze kutoa ushirikiano huyo. Pamoja na hayo, sheria ituambie wazi, kwa sababu huyu mtu anapoenda kufungwa miaka 30, nilikuwa nashauri kabla hajaenda jela hebu tunaomba mtusaidie kabla hajaenda jela aache ametoa fidia kwa huyu mtoto ambaye amempa mimba ili fidia ile iendelee kumsaidia huyu mtoto. Kuwe na alternative kwamba atakayeweza kutoa fidia ile, basi angalau kuwe na unafuu wa ile miaka ya kutumikia jela. Hata kama ana mali, basi zile mali zitaifishwe ili apewe huyu mtoto ambaye amepata ujauzito kwa ajili ya kulea mimba na kwa ajili ya kulea mtoto ambaye anatarajiwa kuzaliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la DNA. Ni kweli kwamba DNA pia tunaomba ifanye kazi, wataalamu watusaidie. Ninavyofahamu ni kwamba DNA ni mpaka mtoto azaliwe. Je, inawezekana kabla mtoto hajazaliwa ili tuone ni namna gani mtu anapohukumiwa asije akatumikia kifungo wakati hajahusika na kosa lile? Tumeshuhudia China kuna mtu alinyongwa kwa kubaka, lakini baada ya miaka 30 hivi akagundulika kwamba siye yeye aliyebaka na tayari alikuwa ameshanyongwa. Kwa hiyo, naomba hilo sheria itusaidie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilikuwa nataka kuzungumza kuhusu ile Sheria ya Matunzo. Sheria ile ilikuwa inasema kwamba matunzo ni shilingi 100/=. Hivi bado inatumika hiyo shilingi 100/=? Wakati ule shilingi 100/= thamani yake ilikuwa kama shilingi 100/= ya sasa hivi. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana sheria hiyo kama haijaletwa, basi iletwe ili iweze kurekebishwa kwa sababu hakuna shilingi 100/= inaweza ikanunua kitu chochote kwa ajli ya matunzo ya mtoto ambaye anakuwa amezaliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba elimu itolewe. Sheria hizi tunapopitisha, wananchi wetu vijijini hawapati elimu ya kutosha, matokeo yake wananyanyasika wakati wana haki ya kuweza kutumia hizi sheria ili ziwasaidie.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa naamua kesi moja kwamba mwanamke anataka kumwacha mume kwa sababu tu amemchoka, lakini mwanaume anamwambia ukinipa talaka wewe, wewe ndio unapaswa kunifidia mimi. Yaani sheria za ajabu ajabu kule zinatolewa. Kwa hiyo, naomba sana sheria hizi ziweze kutolewa elimu kwa wananchi wote ili wote wajue waweze ku-enjoy na sheria hizi nzuri ambazo tunazipitisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia sheria zifanye kazi. Tunapitisha sheria hapa lakini kuna manyanyaso makubwa sana ambayo yanapita. Kwa sababu juzi tu nilikuwa naangalia kipindi cha TBC namna ambavyo mtoto amenyanyapaliwa na baba yake. Hivi hawa wanaume wanaokataa kuwalea watoto wao, wanawakimbia, wanawatelekeza, sheria inasemaje? Vile vile bado kuna wanawake wanatelekeza watoto wao, sheria inasemaje? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba sana pia tuangalie upande huo ili wote waweze kuchukua majukumu yao kwa sababu mtoto yule wameamua kumleta wao duniani na ni lazima alindwe; lakini mtoto wa kike alindwe zaidi na isiwe tu kwa sababu ya wale wanaosoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema chini ya miaka 18, maana sheria naona inamtaja sana matoto aliyeko shule, lakini kuna watoto wengine wanamaliza Darasa la Saba, haendelei, anabaki nyumbani mama au baba wanajitahidi kwamba wanamtafutia mahali pa kwenda, kabla hujapata namna ya kumsaidia, majamaa yameshaingia, wameshampa mimba mtoto na wanaingia mitini. Kwa hiyo, naomba sheria hii imtaje na mtoto ambaye hajafikisha umri hata kama hayupo shule.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na ninaunga mkono hoja, ahsante.
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2016
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na mimi pia kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu alipolihutubia Bunge letu aliona udhaifu na mapungufu ya sheria hii ya manunuzi na ndio maana leo nashukuru Mawaziri wetu wametuletea ili tuweze kuirekebisha kwa manufaa ya Taifa letu. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa nia yake njema ya kuokoa na kuondoa vichaka maana yake sheria hii ilikuwa ni vichaka kwa watu ambao sio waadilifu.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baada ya pongezi hizo mimi sitakuwa na mengi sana kwenye sheria hii kwa sababu sio mtaalamu sana kwenye mambo ya sheria ya manunuzi lakini kuna maeneo mengine ambayo ninaona nitoe ushauri hasa kwenye upande wa afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi ukachanganya hii Sheria ya Manunuzi pamoja na manunuzi ya dawa za binadamu, huwezi ukalinganisha tender ya pembejeo za kilimo au tender ya kutengeneza barabara au tender ya kuagiza vipuli na dawa ambazo zinatumiwa na binadamu. Ninazungumza hivyo kwa sababu sheria hii imekuwa ikichukua muda mrefu sana katika masuala ya uagizaji wa dawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaongea haya labda nideclare interest kwa sababu mimi nilikuwa mjumbe wa Bodi ya MSD, ninafahamu matatizo makubwa ambayo MSD wanayapata namna ya kuagiza dawa kwa kufuata Sheria hii ya Manunuzi. Tender itatangazwa mwezi wa tatu lakini mpaka sasa ukienda bado hata wale ambao wamepata award kwa ajili ya kuleta labda dawa bado kabisa mlolongo ni mrefu, apate zile awarded letter,aje aende apate mkataba, aende kwa AG maana yake na zile kanuni naona walizirekebisha lakini bado hazisaidii aende kwa AG, atoke pale afanyiwe vetting, akitoka kwenye kufanyiwa vetting arudi sasa aende kutoa order na akitoa order dawa ile ikatengenezwe kule kiwandani ni miezi mitatu, kwa sababu MSD wana nembo yao kwa hiyo ni lazima watoe order kiwandani ili zile dawa zitengenezwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba sana Mheshimiwa Waziri hili mliangalie msichanganye hii Sheria ya Manunuzi ya dawa za binadamu na manunuzi ya vitu vingine, ninaomba sana hili mliangalie. Mnaweza mkawa mmeliweka kama mlivyoliweka, lakini hebu mtakapokwenda nendeni mkaangalie na kama mkiona kuna uzito wala msisite lileteni tena hapa ndani ili tuokoe maisha ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninazungumza hayo kwa sababu mimi ninaelewa kwanza kabisa dawa asilimia 80 zinatoka nje, lakini makampuni mengine yanatoka nje yanakuja ku-register dawa hapa, yanapo- register dawa yanasubiri MSD atangaze tender, MSD anapotangaza tender wao kazi yao ni kuvizia na unakuta wana- tender kwa bei ya chini lakini huwezi kujua hata hizo dawa wanakwenda kuzinunua wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa ninaomba sana tuliangalie suala hili na ushauri wangu ni kwamba kuwe na utaratibu kwanza ninashukuru kwamba makampuni ya ndani yanapewa kipaumbele, mimi kwa kweli ninashukuru. Lakini utekelezaji wake, mimi ninawaamini sana Waheshimiwa Mawaziri na watendaji wenu na ninaamini kupitia ile kauli mbiu ya hapa kazi tu. Lakini ninaamini pia kwa kauli mbiu ya kutumbuliwa majipu, nilikuwa ninaomba sana kauli ya utumbuaji majipu uendelee kuangalia ni namna gani makampuni ya Kitanzania hayanyanyaswi. Kwa sababu makampuni ya Kitanzania yananyanyaswa na makampuni ya nje wanakuja na bei za chini kwa kisingizio kwamba Watanzania wananunua vitu vya bei ya chini. Lakini matokeo yake dawa zinazoletwa zinakuwa ni fake wala sio bora kwa Watanzania.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa naomba sana tuangalie bei, lakini lazima uangalie na ubora wa kile kitu unachompelekea Mtanzania hasa kwa afya yake. Kwa hiyo hilo ninaomba sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa sababu hatuna viwanda vya kutosha vya madawa tunategemea viwanda vya nje, nilikuwa naomba makampuni ambayo yanakuwa registered hapa Tanzania ya wazawa au ya nje, wao wawe ni mawakala au ma-agent wa viwanda fulani kule nje ili MSD anapotoa tenda kwa kampuni ile bado atoe copy kwenye kiwanda ambacho yule mtu amesema atatoa zile dawa. Kwa sababu walio wengi wana cheat, watasema kwamba dawa zile wanaenda kuzitoa labda tuseme Malaysia, India au whatever, lakini bado unaweza ukakuta wapo Keko pale wanatengeneza dawa pale, wanaziingiza MSD wakijifanya wamezitoa nje kumbe zile dawa ni fake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nilikuwa naomba kuwe na mahusiano kati ya viwanda ambavyo vimetambuliwa na nchi yetu ambavyo vinatu-supply dawa ili wale ma-agent, wale bidders watuambie zile dawa wakipata tender watakwenda kununua wapi lakini bado copy iende ili tupate bei iliyo sahihi ambayo sio ya kudanganya.Kwa hiyo, mimi niliona nizungumze tu kwenye eneo hili wala sikutaka kuzungumzia sana maeneo mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2017.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami naomba niungane na wale ambao wameendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais, pia nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Kabudi pamoja na

Mwanasheria Mkuu ambao kwa kweli wameonyesha uzalendo mkubwa wa kuweza kusimamia mabadiliko na marekebisho haya kwa manufaa ya nchi yetu ambayo Mheshimiwa Rais amekusudia kuwasaidia Watanzania kutoka mahali walipo ili uchumi wa Taifa hili uendelee kupaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana wewe mwenyewe umeona watu wameshindwa kumpa jina Rais wetu, kuna wengine wanaamua kumtoa kwenye Chama cha Mapinduzi wanataka wamweke kama yeye, hii inaonesha ni namna gani wamemkubali na wana imani naye. Nawapongeza sana na tuendelee kumuunga mkono kwa sababu tumekubali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inanikumbusha wale wanafunzi walipomtembelea Yohana gerezani, Yohana akauliza aliposikia habari za Yesu nendeni mkamuulize je, ni yeye yule au tumtazamie mwingine? Yesu akawaambia, kamwambieni kwamba matendo na yale yote mnayoyaona nendeni mkamweleze yote. Watanzania wameyaona matendo ya Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli wana uhakika kwa matendo tu, inaonesha ndiye ambaye anakuja kulitoa Taifa hili mahali ambapo tumekuwa tukinyonywa hasa kwenye upande wa uchumi na mabepari. Kwa hiyo, tuendelee kumuunga mkono kwa nia yake hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wengine wameonesha wasiwasi wao kwamba, kwa nini mamlaka makubwa yaende kwa Rais, nataka kusema wananchi tayari walishampa mamlaka, lakini kumbukeni yeye ndiye Amiri Jeshi Mkuu wa Jeshi letu la Tanzania, tumemwamini kumkabidhi Jeshi hatuwezi kushindwa kumkabidhi rasilimali za nchi yetu, kwa hiyo, lazima tuendelee kuwa na imani naye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda naomba nizungumzie kuhusu Madini House; tumeona kwamba pamoja na mrabaha utaokuwa unalipwa bado kutakuwa na dhahabu ambayo itakuwa inapelekwa Benki Kuu. Hii naiunga mkono kwa sababu kwanza itaongezea thamani ya pesa yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Madini House naomba madini yote yapite pale, lakini bado naomba wachimbaji wadogo ili waweze kunufaika kama Rais ambavyo amekusudia, pale kuwe na utaratibu wa kwamba Serikali kama ambavyo inaweza ikanunua mahindi kutoka kwa wakulima, ijipange pia kuwe na utaratibu wa kununua yale madini hasa dhahabu kutoka kwa wachimbaji wadogo. Hii itawasaidia sana wachimbaji wadogo wasiweze kuibiwa, kwa sababu wanakuja wale wachuuzi wananunua kwa wachimbaji wadogo, wao wanatorosha madini yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hii itaisaidia sana nchi yetu kwanza kuhifadhi dhahabu ambayo ni nyingi ambayo itasaidia kukuza uchumi wa Taifa letu. Nikiangalia kuna wakati tulikuwa tunapita kwenye migodi yetu, tunakuta wale wachimbaji wadogo wameshika dhahabu mikononi wanaenda watu wanazinunua ndio hao wanaoenda kupita kwenye njia za panya. Kwa hiyo, naomba sana uwepo utaratibu huo ili wachimbaji wetu waweze kunufaika kama Mheshimiwa Rais ambavyo ameunga mkono.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hili kwa sababu natambua shida ambazo tunazo kule kwa wananchi wetu; bado tunahitaji maji, bado tunahitaji madawa, bado tunahitaji watoto wetu waweze kukaa kwenye madarasa mazuri na hii itakwenda kusaidia. Nampongeza Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono.