Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Mariamu Ditopile Mzuzuri (2 total)

MHE. MARIAM D. MZUZURI aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha wakulima nchini kuwekeza katika kilimo cha mazao ya alizeti, michikichi na karanga ili kuokoa kiasi cha fedha zinazotumika kuagiza mafuta kutoka nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Ditopile Mzuzuri, mkulima na mjasiriamali katika sekta ya kilimo kuwa Serikali inaona umuhimu wa kuwekeza kwenye mazao ya kuzalisha mafuta ambapo uwekezaji huo unatekelezwa chini ya mikakati ya kutatua changamoto katika sekta ya uzalishaji wa mafuta kwa kushirikisha Wizara ya Kilimo, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu - Wizara ya Viwanda na Biashara. Mikakati hiyo inalenga kutatua changamoto ya uzalishaji wa mbegu za mafuta ili kujitosheleza kwa mahitaji ya ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2020/ 2021 Serikali imewekeza jumla ya shilingi 5,820,361,798 kwa ajili ya kuendeleza zao la chikichi ambapo kufikia tarehe 31 Januari jumla ya miche bora ya michikichi 2,244,935 imezalishwa na kusambazwa kwa wakulima. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga jumla ya shilingi 3,158,200,000 kwa ajili ya kuzalisha na kusambaza mbegu na miche ya zao la michikichi.

Mheshimiwa Spika, Katika kuhakikisha uzalishaji wa mbegu za alizeti unaongezeka katika mwaka wa fedha 2020/ 2021 Serikali imeiwezesha taasisi ya ASA jumla ya bilioni tatu kwa ajili ya kuzalisha mbegu za alizeti. Vilevile, kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imepanga kuiwezesha ASA shilingi bilioni 10.6 ili kuzalisha tani 5,000 za mbegu ya alizeti kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa mbegu za mafuta

Mheshimiwa Spika, katika kupunguza gharama za kilimo kwa mkulima Wizara imeanzisha miradi ya block farming katika mikoa ya uzalishaji mbegu za mafuta ikiwemo alizeti michikichi na pamba ambapo katika mwaka ujao wa fedha Serikali tutatoa kipaumbele kwa kilimo cha uzalishaji mbegu kwa mfumo wa block farming kwenye baadhi ya mikoa kwa ajili ya uzalishaji mbegu za alizeti, pamba na michikichi. Mahitaji ya mafuta ya kula nchini yanakadiriwa kufika tani 570,000 kwa mwaka. Aidha, uzalishaji wa mafuta ya kula nchini unakadiriwa kufikiwa wastani wa tani 205,000 na kufanya upungufu wa wastani wa tani 365,000 kwa mwaka, ambapo husababisha nchi kutumia shilingi bilioni 474 kuagiza mafuta ya kula kutoka nje ya nchi kwa mwaka.
MHE. MARIAM D. MZUZURI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za viongozi waandamizi wa Serikali kama Makatibu Wakuu na Mawaziri katika Mji wa Dodoma kwa ajili ya makazi ya viongozi hao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Ditopile Mzuzuri, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tangu Serikali kuhamishia shughuli zake makao makuu ya Serikali hapa Jijini Dodoma kumekuwepo na juhudi mbalimbali ili kuhakikisha kuwa viongozi waandamizi wa Serikali wanapata makazi bora ya kudumu na yenye usalama. Katika kutekeleza hilo, Serikali imeanza mkakati wa kujenga nyumba za viongozi katika jiji la Dodoma.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha 2020/ 2021 Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi - Sekta ya Ujenzi, imetenga kiasi cha shilingi bilioni sita kwa ajili ya ujenzi wa nyumba 20 za viongozi na shilingi bilioni nne kwa ajili ya ukarabati wa nyumba 40 za viongozi jijini Dodoma. Hivi sasa kwa kutumia Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) hatua za ubunifu na usanifu wa nyumba hizo pamoja na makadirio ya gharama za ujenzi zimekamilika. Aidha, ukarabati wa nyumba za viongozi jijini Dodoma unaendelea.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi - Sekta ya Ujenzi, imetenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa nyumba 20 za viongozi jijini Dodoma. Aidha, pamoja na ujenzi wa nyumba hizi, Serikali pia imetenga fedha kwa ajili ya kuendelea na ukarabati wa nyumba nyingine 40 za viongozi zilizopo jijini Dodoma katika maeneo ya Kisasa, Area D na Kilimani. Ahsante.