Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Maida Hamad Abdallah (10 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais na Baraza la Mawaziri. Sekta ya Kilimo inayojumuisha uzalishaji wa mazao ya Kilimo, Mifugo, Uvuvi na mazao ya misitu ndiyo tegemeo la maisha ya Watanzania walio wengi.
Hata hivyo, ukuaji wa sekta hii siyo wa kuridhisha sana kutokana na matumizi ya teknolojia isiyoendana na wakati na pia tunategemea majaliwa ya Mwenyezi Mungu katika hali ya hewa. Hata hivyo, tunashukuru hali ya hewa haijawa mbaya sana, kwa zaidi ya miaka kumi tunapata mvua za kutosha na chakula kinapatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu kwa kipindi hiki imedhamiria kuwekeza zaidi katika uchumi huu wa viwanda, uchumi wa viwanda utategemea sana kilimo chetu kwa namna tutakavyojipanga vizuri na mikakati endelevu ya kilimo kwa mazao yetu yenye ubora unaostahili. Kwa kipindi kirefu Mkoani Lindi tumekuwa na mbegu za mazao ya mahindi, muhogo, mpunga, korosho, ufuta, zisizo na ubora. Wakulima wetu wanajitahidi sana kulima mazao haya lakini mavuno yake hayaleti tija kutokana na mbegu isiyo bora lakini na namna ya kilimo cha jembe la mkono.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji sasa Serikali ya Awamu ya Tano kuleta mapinduzi ya kilimo na kuondokana na kilimo cha jembe la mkono, kuwa na mbegu bora na kuwa na kilimo endelevu kwa kutumia pia skimu zetu na mabanio. Tunahitaji Maafisa wa Kilimo watusaidie kutoa elimu ya kilimo bora cha kisasa cha mazao ya biashara, kilimo ni biashara lazima sasa tuondoke tulipo tusonge mbele.
Wakulima wetu wanahitaji kupewa elimu, kupata mbegu bora na pembejeo za kilimo kwa wakati, Serikali ni vema ikajipanga kujua mahitaji ili vijana wetu na wanawake waweze kupata ajira na kuweza kukuza vipato vyao kupitia kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Lindi Manispaa tunalo banio limejengwa kwa pesa nyingi sana lakini bado halijawanufaisha wakazi wa Kata ya Ng‟ape, sasa lina zaidi ya miaka mitatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu korosho; korosho ndiyo zao la biashara katika Mkoa wa Lindi, kumekuwa na tatizo kubwa la upatikanaji wa fedha wakati wa mauzo ya korosho, Vyama vya Ushirika vinawakandamiza sana wakulima hata kama bei elekezi inatolewa. Tunaiomba sana Serikali kutusaidia kusimamia Vyama vya Ushirika, wakulima wetu wamekuwa maskini kwa kipindi kirefu na hawana msaada wowote.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yangu ina dhamira njema ya mfumo wa stakabadhi ghalani, lakini kwa namna unavyoendeshwa wakulima wanapata kero ya kutopata fedha zao kwa wakati na wapo watu wanatajirika kwa mfumo huu hasa wanaoendesha Vyama vya Ushirika na wakulima wanaendelea kuwa maskini na kukatishwa tamaa na Serikali yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Sekta ya Uvuvi; Mkoa wa Lindi wakazi walio wengi ni wavuvi, maeneo ya Kilwa, Lindi Vijijini na Lindi Manispaa uvuvi uliopo hauna tija. Changamoto kubwa ni pamoja na:-
(i) Kutokuwa na zana bora za uvuvi;
(ii) Kutokuwa na elimu ya uvuvi;
(iii) Kutokuwa na boti zenye engine wakaweza kwenda masafa marefu kwa ajili ya kuvua; na
(iv) Masoko ya uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri ni kwamba, tunaiomba Serikali kutusaidia Mkoa wa Lindi, vijana wetu wakaandaliwa katika vikundi na wakawezeshwa kufanya shughuli za uvuvi ili kuleta ajira kwa vijana na kuleta ustawi wa wananchi wa Lindi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa kazi nzuri anazofanya na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
HE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii. Naipongeza sana Serikali kwa juhudi zake za kuleta maendeleo nchini. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu wake na timu yake yote ya wataalam inayowasaidia kutekeleza kazi zao vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja niende kwenye utaratibu wa kupunguza umaskini. Vigezo vya MKUKUTA I na II ni kuwa na wastani wa kila mtu kutoka Sh.770,464.3 mwaka 2010 hadi Sh.1,918,928/= mwaka 2015 kwa mujibu wa Mpango wa Taifa 2016/2017. Pia kasi hiyo inaendana na matarajio ya kutoka asilimia 24.5% iliyokuwepo mwaka 2015 na kushuka hadi kufikia 16.7%. Njia kubwa ya kuondoa umaskini ni pamoja na kujitosheleza kwa chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu kwamba upatikanaji wa chakula kwa wingi chanzo chake ni upatikanaji wa mbegu bora, tafiti na umwagiliaji na bajeti ya kutosha kwenye mahitaji ya kilimo. Ni kwa nini bajeti ya kilimo inaendelea kutengwa ndogo ambapo inahitaji mipango ambayo inaweza kuendeleza kilimo na kuweza kujitosheleza kwa chakula ili kuondoa umaskini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanafunzi au wahitimu waliochukua mikopo kwa ajili ya kujiendeleza. Wahitimu hawa waliingia mkataba na Bodi kwa kukubali kulipia 5% baada ya kumaliza masomo bila riba. Jambo la kusikitisha au linalowashangaza wengi ni kwa nini wameitwa wadaiwa sugu wakati wengi wao wapo kwenye Wizara za Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili Serikali imewashtukiza kwa kuongeza riba ya kutakiwa kulipa asilimia 15 badala ya 5% iliyokuwa awali. Ni kwa nini kwa vile wapo kwenye Wizara, Serikali isiwe inakata marejesho ya mikopo hiyo bila riba baada ya kurudi kwenye Wizara zao? Sheria ya kuongeza riba kwa mikopo hiyo ni kuwapa adhabu, kwani wengi wao ni maskini sana, hawana uwezo wa kifedha na hawataweza kujiendesha kimaisha. Ni vema kubaki na 5% kama awali ya mikataba yao inavyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilitoa kauli kwamba mwaka 2015, Benki ya Wanawake ilifikia mtaji wa shilingi bilioni 20, lakini pia ilifungua vituo vya kutoa mafunzo na mikopo katika mikoa mbalimbali, jumla ya wananchi 12,874 wakiwemo wanawake 9,693. Nataka kujua miongoni mwa wananchi waliopatiwa elimu hiyo kwa upande wa Zanzibar, imejipanga vipi? Kwani mtaji wa Benki ya Wanawake, baadhi ni michango ya hisa za Waheshimiwa Wabunge toka Zanzibar na hati za uthibitisho zimetolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Pamoja ya Fedha, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, kwa ujumla mashirika tisa yanayotekeleza masuala ya Muungano kwa sehemu kubwa mtaji wake ulitokana na Tanzania bara. Ni kweli, swali, je, kama mtaji umetokea upande mmoja wa Muungano, lakini upande wa pili ukawa umewekeza na rasilimali, taratibu za kimapato kwa mujibu wa sheria za nchi na Katiba ya 1977 zinasemaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ili na mimi nichangie machache katika bajeti hizi za Wizara mbili. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia jioni hii ya leo kusimama katika Bunge hili na kuchangia bajeti iliyoko mbele yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kuhusu ufinyu wa bajeti. Takribani Wizara zote katika bajeti hii zimekabiliwa na ufinyu mkubwa wa bajeti. Kwa hiyo, ni vyema Serikali katika vyanzo vyake vya mapato vilivyopo na vile ambavyo inaendelea kuvibuni siku hadi siku ndani ya bajeti hii iweze kufikiria Wizara tofauti tofauti, hizi tunazozijadili na kuwaongezea ili ziwe na bajeti za kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua majukumu waliyonayo Wizara hizi lakini pia nataka nijikite katika Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma pamoja na ile Tume ya Ajira. Tume hizi zimekuwa zikifanya kazi kwa nguvu zote kwa maslahi ya wananchi na viongozi wa umma walioko katika nchi hii. Tume hizi zimekuwa zikikabiliwa na ufinyu wa bajeti mkubwa na zaidi majengo au ofisi wanazofanyia kazi ni za kupangisha kwa bei ya juu. Vitendea kazi vya kutosha hawana na ukiangalia bajeti yao ilivyo na ukiangalia mahitaji ya fedha ambazo zinatakiwa kulipwa kwa ajili ya ofisi wanazofanyia kazi basi utashangaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunatembelea ofisi hizi, kuna Mheshimiwa mmoja wakati wanatoa changamoto zao alijitolea kuchangia kompyuta pamoja na vifaa vyake. Hii ni aibu jamani, sisi tunakwenda kule kuwapa ushauri na mambo mengine lakini pia sisi sio watu wa kuchangia vifaa vya ofisi hizi wakati ofisi hizi ni muhimu sana katika Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma imekuwa ikifanya kazi kwa nguvu zote, lakini pia cha kusikitisha bajeti yake yote ikiwemo mishahara ya watumishi ni ufadhili kutoka nje, inasikitisha sana. Ni vema Serikali ikajitahidi na ikajikita katika suala la kuongeza bajeti katika ofisi hizi. Mara nyingi tumekuwa tukiwalaumu, tukiwakosoa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwamba hawatekelezi majukumu yao lakini kumbe hawana bajeti, hawana ofisi ya kufanyia kazi, wana-share ndani ya ofisi, wanakaa nje, hawana sehemu nzuri za kufanyia kazi, hawana vifaa vya kutosha lakini pia yote haya yanatokana na ufinyu wa bajeti unaozikumba ofisi hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niende moja kwa moja katika mikoa na Halmashauri husika. Waheshimiwa Wabunge wengi hapa wamechangia na kusema kwamba asilimia 30 ya kodi ya majengo ndani ya Halmashauri hazirejeshwi. Wanajitahidi kukusanya kodi hizi lakini pia mrejesho unakuwa hauwafikii. Serikali imewapangia makusanyo kupitia vyanzo vyao vya mapato asilimia 30 kwa mujibu wa bajeti na Halmashauri zimekuwa zikijitahidi sana kukusanya lakini leo kutokana na kuwa hawana mrejesho katika makusanyo kama haya au kodi hizi kwa hiyo imefikia hatua hawawezi kutumia au hawawezi kufaidika na fedha hizi. Pia Halmashauri zetu zina upungufu wa Maafisa Ugani, zina upungufu wa wataalam wa kilimo na hakuna watafiti wa kilimo. Kwa hiyo, ni vyema tukazipa uhuru Halmashauri hizi ili ziweze kujitegemea na kile wanachokikusanya pia tusiwabane sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuweka mfumo sahihi wa matumizi ya electronic kwa kusambaza vifaa vya electronic katika Halmashauri zote ili kuhakikisha kwamba mapato ndani ya Halmashauri hayawezi kuvuja. Yote yanatokana na kuwa hakuna mashine za electronic na ndiyo maana tukaona mapato yanapotea siku hadi siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie suala la wastaafu. Mara nyingi wastaafu wamekuwa wakiilalamikia Serikali kwamba wanapata usumbufu mkubwa katika kufuatilia haki zao. Baadhi ya changamoto wanazozieleza wastaafu moja ni kutokana na kuwa waajiri hawatekelezi wajibu wao kwa wale wafanyakazi ambao wamejiunga na Mifuko ya Hifadhi jamii ambapo wanakuwa hawafikishi fedha zile mpaka inafikia mfanyakazi anafikia kustaaafu. Pia kuna tatizo la kuchelewa kufikisha nyaraka Hazina. Yote haya inawasababishia wastaafu kuchelewa kupata haki zao na kuja kupata usumbufu baada ya kustaafu. Niiombe sana Serikali kuwafikiria kwanza wastaafu hawa au wastaafu watarajiwa na kuwaomba hizi ofisi kwamba itakapofikia mtu karibu na kustaafu ndani ya miezi mitatu kabla basi nyaraka ziweze kufikishwa mapema kunakohusika ili wastaafu hawa itakapofikia kustaafu waweze kufaidika na wasipate usumbufu. (Makofi)
Kuhusiana na suala la MKURABITA, niipongeze sana Serikali kwa jitihada zake za kufanikisha na suala hili. Pia nitoe pongezi kwamba imeenea katika maeneo mengi Tanzania Bara na kule Zanzibar, wengi wameweza kupimiwa maeneo yao na kupata hati miliki za kimila. Pia niombe sana Serikali kupitia hati hizi za kimila kwa vile tumefungua Benki ya Kilimo wananchi waruhusiwe kuzitumia kama dhamana pale wanapohitaji mikopo kwa ajili ya kuendeleza kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye TASAF, mfuko huu ni muhimu sana katika Taifa letu lakini cha kusikitisha pamoja na kazi kubwa inayofanywa lakini pia jamii ni pamoja na wananchi waliotuzunguka katika Majimbo yetu. Sisi Wabunge mara nyingi hatujui nini mfuko unafanya wala kushirikishwa maendeleo yanayopatikana na hata tukihoji basi inakuwa ni kazi ngumu kupata majibu. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali iwashirikishe Wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wawe wa Viti Maalum au wa Majimbo katika maeneo wanayotoka kushirikishwa kwa miradi yote na kwa namna yoyote au hata katika Kamati za TASAF zinazopanga utaratibu mzima kuhusiana na masuala yale ya kijamii na uwezeshaji wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, nakushukuru sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia katika bajeti hii ya Serikali ya mwaka 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kusimamia uchumi wa Taifa hili. Tunampongeza Mheshimiwa Rais na tunasema Watanzania wengi tupo nyuma yake, aendelee na kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza pia Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii wakiwemo pamoja na wataalam waliosaidia kwa njia moja au nyingine hadi kukamilika kwa bajeti hii ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti pia niwapongeze wananchi wa Tanzania waliopongeza au wanaoendelea kupongeza bajeti hii ya Serikali, bajeti hii ni nzuri na ina matumaini makubwa kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nithubutu kusema kwamba wananchi wa Tanzania wengi ni wa kulima na wameipongeza bajeti hii kwa sababu imeweza kuwafutia kodi mbalimbali katika ushuru mbalimbali wakiwemo wakulima, wafugaji wamefutiwa kodi za mazao, wamefutiwa kodi kwenye chakula cha mifugo, wamefutiwa kodi katika vifaranga lakini pia nithubutu kusema kwamba wananchi hawa wameendelea kupongeza Serikali hasa pale mkakati wa Serikali wa usambazaji wa mradi wa umeme vijijini.

Lakini pia wananchi hawa, wamekuwa wakipongeza Serikali kwa kufutiwa gharama za service charge katika gharama za umeme, kwahiyo, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais, kwa jitihada zake za kuleta au kwa kuwarahisishia wananchi uchumi ulio nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali kwa vile wananchi wengi ni wa kulima katika Taifa hili, na Serikali kupitia sekta yake ya kilimo au kupitia sekta ya kilimo imekuwa ikiandaa mikakati mbalimbali ya kukuza kilimo lakini pia imekuwa tofauti katika kufikiwa malengo ya kilimo kutokana na uchache wa fedha.

Kwa hiyo, basi niiombe sana Serikali kupitia sekta ya kilimo kuingiza fedha haraka au Hazina wapeleke fedha haraka ili sekta yetu ya kilimo iweze kukua na ile mikakati iliyopangwa ya kukuza kilimo iweze kufikiwa na tuweze kukuza uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja niende katika Benki ya Wanawake. Katika vitabu vya Serikali vile vya mpango pamoja na vya bajeti vimekuwa vikieleza kwamba sasa hivi Benki hii imekuwa ikiendelea katika maeneo mengi katika Tanzania Bara, na imeshafungua vituo na imeshaanzisha vituo karibuni 252 katika maeneo ya Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nithubutu kusema kwamba benki hii uanzishwaji wake tulishiriki wananchi mbalimbali na wafanyabiashara mbalimbali waliopo Tanzania Bara na Zanzibar. Lakini pia kuna hisa walizonunua au walizowekeza katika Benki hii, hadi leo benki imekuwa ikiendelea kufungua vituo au matawi katika maeneo ya Tanzania Bara lakini Zanzibar wamekuwa wakichelewa kuhusiana na suala la ufunguaji wa vituo hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Serikali kuendelea pamoja na kuwa inaendelea Tanzania Bara lakini pia iendelee kufungua vituo Tanzania Zanzibar kwa sababu Zanzibar kuna wananchi wajasiriamali, Zanzibar kuna wakulima, Zanzibar kuna wafugaji na wao wanahitaji mikopo kupitia benki hii na benki hii haianishi wanawake tu inakwenda moja kwa moja kwa wananchi wote katika jamii. Kwahiyo, niiombe sana Serikali kujielekeza kule Zanzibar kufungua vituo Unguja na Pemba ili nao waweze kufaidika na hisa walizoziweka viongozi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nilitaka nizungumzie kuhusu shilingi 40 zilizowekwa katika lita ya mafuta, wananchi hawajaona tatizo kuwekwa shilingi 40 kila lita moja ya mafuta kwa sababu kodi mbalimbali walizokuwa wanalipa ilikuwa ni zaidi ya shilingi 40. Kwa hiyo wamefurahi na hawana tatizo ya lita ya mafuta kuongezeka shilingi 40, shilingi 50 haitumiki hata ukienda dukani basi huwezi kutumia shilingi 50 wala hawaoni tatizo shilingi 40 kwa kila lita ya mafuta kuongezwa katika suala la ulipaji wa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niiombe sana Serikali pamoja na kuwa imewajali wakulima, lakini pia iwajali na wafanyabiashara, kuna wafanyabiashara wakubwa, kuna wafanyabiasha wadogo. Pia wafanyabiashara hawa wamekuwa na utitiri wa kodi, utitiri wa kodi kwanza kulipia mzigo bandarini, wanaposafirisha mizigo yao kupeleka dukani, wanapofikanao mzigo huu dukani na kila wanapouza bidhaa zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na kuwa Serikali au Mheshimiwa Rais amefikiria suala la wakulima lakini pia lifikirie na wafanyabiasha kwa sababu wafanyabiashara wengi kodi zimekuwa kubwa, imekuwa wamefunga biashara zao na walikuwa wanaajiri watumishi mbalimbali, kundi kubwa la vijana sasa hivi halina kazi wafanyabiashara wamekuwa wakifanya kazi wenyewe na kuwaacha wafanayakazi wao. Kwa hiyo, wengi wa vijana hawa baada ya kukosa kazi wameingia katika masuala ya ubakaji na hujuma mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo, niiombe sana Serikali pamoja na kuwa katika bajeti hii tumewafikiria sana wakulima lakini tuwafikirie na wafanyabiashara kwa sababu ndio wanaongeza uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusiana na suala la mapato ya fedha yanayotokana na watumishi wa Jamhuri ya Muungano walioko Zanzibar. Mpaka leo hii na suala hili limekuwa muda mrefu sasa, kusanyo la shilingi bilioni 1.75 hili ni suala la muda mrefu, kwa hiyo, mishahara hii imekuwa ikikuwa siku hadi siku wamekuwa watumishi hawa wakiongezewa mishahara, kwa hiyo, niiombe sana Serikali kufanya tena mchakato au tathimini ya wafanyakazi walioko Zanzibar kutoka kipindi cha nyuma hadi sasa hivi wameongezeka kwa kiasi gani, lakini pia mapato yanayotakiwa kuingia sasa hivi Zanzibar kuhusiana na watumishi hawa income tax ni kiasi gani tusiendelee tu na asilimia 1.7 kama tunavyoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nipewe elimu kuhusiana na suala la asilimia 4.5 inayoendelea kwa sababu asilimia hii 4.5 ni ya muda mrefu kwa upande wa Zanzibar wananchi wamekuwa wakituuliza maswali mengi, kwa hiyo niiombe sana Serikali kutoa elimu zaidi kwa sababu uchumi toka tulipo ingia katika Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kuwa Tanzania ni muda mrefu, uchumi wetu umekuwa ukikua siku hadi siku, tofauti na uchumi ulivyokuwa nyuma, kwa hiyo, asilimia 4.5 naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya majumuisho atupe elimu kuhusiana na asilimia 4.5 ili wananchi wa Zanzibar waweze kuridhika na wasiwe na maswali kuhusiana na maswali kuhusiana na kero za Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba ambayo iko mbele yetu. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uwasilishaji wa taarifa yake ya utekelezaji kwa kipindi hiki cha 2019/2020, hotuba ambayo imesheheni mambo mbalimbali ambayo yametekelezwa lakini na mwelekeo wa Serikali katika kukuza uchumi wetu na katika kutekeleza Mpango wa Miaka Mitano ambao tutaumalizia mwaka kesho.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa namna ambavyo anajitoa na namna ambavyo anatumikia Serikali hii lakini kwa namna ambavyo anawajali wananchi wake wa Wilaya ya Ruangwa kule Jimboni kwake. Pamoja na kwamba ana majukumu makubwa ya kitaifa lakini anapopata fursa hata ya siku moja, mbili anakimbia na kwenda kuungana na wananchi wake katika Jimbo lake la Ruangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Makamu wake wa Rais kwa namna ambavyo wanasimamia utekelezaji wa miradi mikubwa na kuona ni namna gani wanaendelea kukuza fursa za uchumi katika nchi yetu lakini kuendelea kukuza uwekezaji kwa kutekeleza hii miradi mikubwa. Tumeona namna ambavyo ujenzi na upanuzi wa barabara pamoja na madaraja makubwa ambayo yanajengwa katika kuhakikisha kwamba Watanzania tunasafiri bila matatizo yoyote kutoka mkoa mmoja kwenda mkoa mwingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wetu wa Lindi tumebahatika kipindi kilichopita tulitenga fedha kwa ajili ya kujenga barabara inayotoka Nanganga – Luchelegwa – Nachingwea - Masasi. Wananchi wa Wilaya hizi tumefarijika sana kuona kwamba tulitengewa fedha. Mpaka sasa ujenzi haujaanza napenda kujua wamekwama wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kwamba Serikali imeendelea na ujenzi wa reli ya Standard Gauge ambayo inaendelea vizuri. Kwa speed inayokwenda nayo nina hakika kabla hatujamaliza Bunge hili na sisi tutakuwa tumeshuhudia namna ambavyo reli hizi za kisasa zinafanya kazi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona pia upanuzi wa bandari ya Dar es Salaam kule Tanga na Mtwara. Upanuzi huu wa bandari umetoa fursa kubwa kwa wananchi wa Mikoa hii ya Kusini kwa sababu sasa nafasi za ajira kwa vijana wetu zinaongezeka kwa kutumia bandari ya Mtwara. Si hivyo tu hata wafanyabiashara wanaouza mafuta sasa wanapata urahisi wa kupokea mafuta kutoka Mkoa huu wa Mtwara kwa sababu ya upanuzi wa bandari ile ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishukuru pia Serikali imeendelea kuboresha kwa kujenga vituo vya afya na hospitali na kuboresha zahanati katika maeneo mbalimbali. Sisi katika Mkoa wa Lindi tumebahatika katika Majimbo yote tumepata vituo viwili viwili katika kila Jimbo na viko kwenye hatua nzuri sana na vingine viko tayari kwa ajili ya ufunguzi. Nachoiomba Serikali kufanya maandalizi sasa ya watumishi pindi vituo hivi vya afya vitakapokamilika basi tuwe na watumishi wa kutosha wa kusimamia vituo vyetu vya afya ili kuendelea kuboresha afya kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kwa kuongeza uzalishaji wa umeme kupitia mradi wetu wa Stigler’s Gorge. Nimebahatika kutembelea eneo la mradi wa huu, kwa fedha iliyotoka kwa hakika mradi unekwenda vizuri sana. Naomba Mheshimiwa Rais wetu asirudi nyuma katika kuhakikisha kwamba mradi huu unafanikiwa na hatimaye tuweze kuwa na umeme wa kutosha kwa sababu uwekezaji unategemea sana uwepo wa umeme katika nchi yetu. Kwa hiyo, umeme huu utakuwa ni mkombozi mkubwa sana na uwekezaji utakuwa ni mkubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia kuipongeza Serikali, kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa ujasiri ambao ameuonesha katika ununuzi wa ndege, maana sasa tunapata heshima kubwa katika nchi yetu kumiliki ndege zetu wenyewe. Hilo ni jambo la faraja sana, ni jambo jema katika kukuza uchumi na kuendelea kuimarisha uwekezaji katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie katika Mkoa wetu wa Lindi. Katika Mkoa wetu wa Lindi sasa tumefungua fursa za uwekezaji. Kwa hiyo, ninaomba sana ushirikiano na Serikali kuhakikisha kwamba eneo hili la uwekezaji katika Mkoa wetu wa Lindi tunafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo maeneo mbalimbali kwa kila Wilaya, kuna fursa mbalimbali za uwekezaji, nami nitumie nafasi hii kuwaalika Waheshimiwa Wabunge mbalimbali, karibuni kwetu Lindi, mje kujionea, yawezekana nanyi mkabahatika au mkapenda kuja kuwekeza katika maeneo mbalimbali ilimradi katika Mkoa wetu wa Lindi tuendelee kukuza uchumi wetu, lakini tuweze kutengeneza ajira mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wetu wa Lindi tuna viwanda vidogo vidogo na nina hakika kwa nafasi hii tumekuwa tukiongoza kwa kuwa na viwanda vingi vidogo vidogo vinavyofikia karibu 400 na zaidi. Viwanda hivi vyenye ajira kuanzia mtu mmoja, wawili, watatu; kwa hiyo, SIDO Lindi wamefanya kazi nzuri maana viwanda hivi vimetokana na mafunzo ambayo SIDO wameweza kuyasimamia katika kuhakikisha wananchi wa Mkoa wa Lindi wanaweza kupata ajira kwa kujiajiri wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba sana Serikali kuhakikisha kwamba tuendelee kuwasaidia SIDO Lindi ili waendelee kufanya kazi zao za kuendelea kutoa mafunzo mbalimbali katika maeneo mbalimbali kuhakikisha kwamba wananchi wa Lindi wanaendelea kuingia katika eneo hili la viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali katika kukuza utalii katika Mkoa wa Lindi kwamba tunao mji mkongwe wa Kilwa, mji ambao ulianza kutumia sarafu yake wenyewe katika eneo hili la Afrika Mashariki. Kwa hiyo, yako mambo mbalimbali ambayo tukiyasimamia yanaweza yakatuletea fedha nyingi za kigeni na kuwavutia watu mbalimbali kuja kutembelea katika eneo hili la Kilwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba Vita vya Maji Maji vilianzia pale Kilwa katika Kata ya Kipatimu. Eneo lile lina historia yake kwa sababu, ndugu zetu Wakoloni walikuwa wanashangaa namna ambavyo Kinjikitile Ngwale aliweza kutengeneza jambo ambalo lilifanya Wakoloni watupige risasi za moto maana yake zinabadilika na kuwa maji. Kwa hiyo, ni historia kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna kila namna ya kuukuza utalii katika eneo hili, kwa sababu ndugu zetu Wakoloni waliweza kukata kichwa cha Kinjikitile Ngwale na kupeleka kwao kwenda kuchunguza kwamba mtu huyu, utaalamu huu amewezaje kubadilisha risasi ya moto na kuwa maji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuna kila namna ya kukuza utalii katika eneo hili. Maana ya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa. Muda wako umekwisha. Ahsante sana.

MHE. MAIDA H. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee, nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi zake kubwa sana kuleta maendeleo ya Watanzania. Awamu hii ya Tano wananchi wameweza kuona utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo iliyosimamiwa na Serikali kupitia usimamizi bora wa fedha za ndani. Watanzania kwa ujumla wameanza kufahamu umuhimu wa ulipaji kodi na athari zitokanazo na kutolipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba Serikali iendelee kutoa elimu kwa walipa kodi kupitia vyombo mbalimbali na kuchukuliwa hatua za kinidhamu wakwepaji kodi. Pia usimamizi zaidi wa fedha uimarishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iendelee kusimamia wafanyabiashara ambao bado wanaendelea kutumia risiti za mkono na kukwepa matumizi ya risiti za kielektroniki. Kumekuwa na baadhi ya wafanyabiashara huwalazimisha wanunuzi kulipa bei ndogo bila risiti za kielektroniki na bei kubwa kwa risiti, hivyo, malengo ya makusanyo ya fedha kutokufikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti iliyopita tumeweza kuona upungufu katika fedha iliyopangwa kutolewa na wafadhili katika miradi ya maendeleo na kusababisha baadhi ya miradi kutokukamilika. Naiomba Serikali kutekeleza mpango wake madhubuti wa ushirikiano wa wadau wa maendeleo ili kuendelea kupokea misaada na mikopo kwani bado hatujaweza kusimama wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, vipaumbele; pamoja na vipaumbele vilivyoainishwa katika bajeti hii ambapo njia na vyanzo muhimu vya mapato ya Serikali nashauri:-

(1) Kilimo na mifugo viongezewe fedha zaidi ili kuimarisha mapato zaidi ya Serikali.

(2) Utafiti uboreshwe kwa kutengewa fedha ya kutosha.

(3) Uvuvi wa Bahari Kuu uainishwe katika vipaumbele vya bajeti kwani tunapoteza rasilimali nyingi sana wakiwemo samaki kupitia meli za nje wanazovua katika mipaka yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kuangalia namna itakavyowezekana kuhusu baadhi ya sheria ambazo zinatofautiana na Zanzibar na kuleta vikwazo kwa wananchi na wafanyabiashara wa Zanzibar na kwingineko nchini. Utaratibu bora ufanyike ili kuwawekea mazingira mazuri ya kibiashara na kuondoa kero zisizokuwa za lazima kila mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunaamini na kutambua kwamba biashara ndiyo miongoni mwa vyanzo vikuu vya mapato ya Serikali. Juhudi za Mheshimiwa Rais kukutana na baadhi ya wafanyabiashara tunaendelea kuzipongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo machache, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kusamehe jumla ya shs. 22 billion za Kodi ya Ongezeko la Thamani kupitia umeme unaonunuliwa na Shirika la ZECO Zanzibar. Kitendo hiki kimewatia moyo sana wananchi wa Zanzibar. Naiomba Serikali iendelee kutatua baadhi ya kero zinazowaletea adha wananchi kadri pale uwezo utakaporuhusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, niendelee kuipongeza Serikali kwa kuondoa tozo mbalimbali zilizokuwa zinakwaza wananchi. Ni ushahidi tosha kwamba Serikali yetu ni sikivu na inajali wananchi wake. Hongera sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Mgufuli, hakika wewe ni mtetezi wa wanyonge.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kutilia nguvu suala la utafiti ili kukuza na kupanua uchumi katika nyanja mbalimbali kwa uhakika.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia hoja iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kwa namna ya pekee, kwa vile nimesimama kwa mara ya kwanza, nimpongeze Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lakini pia nimpongeze kwa hotuba anazoendelea kuzitoa tokea kuapishwa kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kwa namna ya pekee nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa hotuba yake ya juzi, Mei Mosi, kwa kuongeza umri wa wategemezi kutoka miaka 18 hadi miaka 21. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiendelea, nataka nizungumzie kuhusu suala la upungufu wa askari. Moja kwa moja nataka nijielekeze katika Mkoa wetu wa Kaskazini Pemba. Tunafahamu kwamba askari wanafanya kazi kubwa sana na wanatusaidia kwa njia moja au nyingine katika kulinda raia na mali zao.

Mheshimiwa Spika, katika mkoa wetu, askari ni wachache na uchache huo umetokana na kwamba wengi wamestaafu, wengine wamepandishwa vyeo, wengine wamefariki na wengine wamepata uhamisho kutoka kituo kimoja kwenda kituo kingine, na hata nje ya Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa askari hawa, kutokana na umuhimu wa mahitaji tuliyonayo ndani ya Mkoa wa Kaskazini Pemba, ingawaje wengi wamechangia katika maeneo au kwa nchi nzima kwamba askari ni wachache, lakini kwasababu nimejielekeza Mkoa wa Kaskazini Pemba, niseme tu kwamba tunaomba tuongezewe askari katika maeneo yetu kwa sababu askari ni wachache.

Mheshimiwa Spika, suala la nyumba za watumishi; naipongeza sana Serikali kwa kuongeza bajeti ya kuendelea kujenga nyumba za watumishi. Ndani ya Mkoa wa Kaskazini Pemba, yapo majengo ambayo Serikali kupitia Wizara hii imeendelea kujenga lakini bado askari wetu wana upungufu wa makazi; askari wetu wengi wanakaa uraiani. Niiombe sana Serikali kuongeza bajeti au kuweka uharaka katika kuendelea kujenga majengo haya ili askari wetu waendelee kuondokana na changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la OC; OC bado ni ndogo, lakini hata hiyo inayotengwa bado haiwafikii walengwa. Niiombe sana Serikali kwa vile kupitia Wizara ya Afya pamoja na Elimu, fedha zinaelekezwa moja kwa moja kwenye vituo, basi niiombe sana Serikali fedha hizi za OC ziende moja kwa moja kwenye vituo husika ili kuondosha changamoto kwa sababu madeni yamekuwa ni mengi.

Mheshimiwa Spika, wana madeni mengi ya mafuta, hawawezi kutekeleza majukumu yao kutokana na uchache wa mafuta, uchache wa vifaa. Kama OC itakwenda moja kwa moja na itakwenda kwa wakati, basi wataweza kulipia madeni yao kwa wakati, lakini pia wataweza kufanya kazi zao kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kuhusiana na suala la fedha ambazo zilikuwa zinatengwa kwa ajili ya kuwahudumia askari hawa, zile shilingi laki tatu kwa miezi mitatu, na hii ni kutokana na uanzishwaji wa maduka ya duty free. Askari hawa walikuwa wanapatiwa huduma katika maduka haya kuweza kujikimu kimaisha.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi Serikali imesitisha lakini kutokana na hilo Serikali ikawa imetenga kila mwezi angalau askari hawa waweze kupewa laki moja kwa ajili ya kujihudumia kiuchumi. Pamoja na hilo, fedha hizi zikawa zinatengwa shilingi laki tatu kwa miezi mitatu, yaani ili kufidia kwamba hatuwezi kuwapelekea kila mwezi lakini tuwe tunawapelekea kwa miezi mitatu; hata hilo pia limekuwa na changamoto. Muda mrefu hawakuwa wakipokea fedha hizi, naomba sana Serikali askari hawa tunajua kazi wanazozifanya, hizi lakini tatu ziweze kuwafikia kwa haraka ili waweze kutekeleza majukumu yao.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Maida Hamad Abdallah.

MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante, nashukuru.

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia uzima wa afya na kuweza kuandika mchango huu kwa njia ya maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali chini ya uongozi wake Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuleta bajeti hii iliyolenga kuwapa matumaini wananchi wa Tanzania kwa kuondoa baadhi ya changamoto zinazoendelea kuwakabili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba bila makusanyo ya kodi hatuwezi kufika mbali kimaendeleo wala hatuwezi kutekeleza miradi ya maendeleo tunayopanga. Lazima wananchi wa Tanzania waweze kuwa na uelewa mpana kuhusu uwajibikaji na wigo wa kukubali kukusanya kodi kupitia wafanya biashara wakubwa na wadogo nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa sio waaminifu katika kutumia mashine za kielektroniki. Wamekuwa wakisingizia kuwa ni mbovu au kukusanywa na TRA. Jambo hili limekuwa likidhoofisha sana ukusanyaji wa mapato ya Serikali. Tumekuwa na juhudi kubwa kama wananchi wa Tanzania tunaponunua bidhaa madukani kudai risiti, lakini kwa muda mrefu sasa wafanyabiashara walio wengi wamekuwa hawatoi risiti wanapofanya mauzo. Niiombe sana Serikali, usimamizi iliyoueleza kupitia hotuba hii ya bajeti iwahusishe wafanyabiashara wote waliostahili kutumia mashine za EFD.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yetu kwamba wale wote wanaopaswa kutumia mashine za kielektroniki watatekeleza wajibu wao lakini pia wanaopaswa kusimamia ukwepaji kodi kwa wafanyabiashara hawa wataweza kusimamia ipasavyo. Pia ni mategemeo ya wananchi kwamba vyanzo vipya vilivyoainishwa kukusanywa kupitia mafuta na miamala ya simu itaweza kukusanya ipasavyo na kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyopangwa. Wananchi hawana maswali mengi pale wanapoona fedha yao inayochangwa na kukusanywa na kuona kwa uhalisia utekelezaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jambo lililokuwa changamoto kubwa kwa wananchi ni suala la tozo kwa bidhaa hata za nyumbani kuendelea kutozwa kodi. Ni furaha ilioje kwa wananchi wa Tanzania kuona bajeti hii imekuja kuondoa kabisa changamoto hii. Ni imani ya wananchi kwamba zile changamoto nyingine zilizobaki zitaweza kufanyiwa kazi hatua kwa hatua. La msingi wananchi tujitahidi kuchangia makusanyo ya kodi ili fedha itayopatikana iwe mfano wa kutekeleza miradi ya maendeleo iliyopangwa ili bajeti ijayo iweze kutatua changamoto nyingine zilizobaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi wananchi wamekuwa wakihoji kuhusu fedha za Jamhuri ya Muungano kupitia Mfuko wa Pamoja wa Fedha. Niwaombe tu wananchi wa Zanzibar kuangalia miradi inayoendelea kutekelezwa kwa upande wa Zanzibar kupitia Mfuko wa Jamhuri ya Muungano na kufuatilia gharama ya fedha zilizotumika kupitia miradi hiyo. Hii nchi ni moja na utekelezaii wa miradi unaendelea vizuri, muhimu tuendelee kulipa kodi kwa manufaa ya Watanzania wote. Tuendelee kusimamia mapato yanayotokana na kodi kwa manufaa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo machache naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii adhimu ya kuchangia hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya na ya kupigiwa mfano ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa taasisi hii ambao wanafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha kwamba sekta hii ya ardhi inapata mapato ya kutosha na kuweza kuwatatulia wananchi kero zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika makusanyo ya maduhuli. Wizara katika kipindi cha mwaka 2022/2023 ilijipangia kukusanya shilingi bilioni 250 kutokana na vyanzo vyake vya mapato. Uhalisia wa mapato hayo waliweza kukusanya asilimia 42.55 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi hiki cha mwaka 2023/2024, Wizara pia imeweza kujipangia kukusanya jumla ya shilingi bilioni 300. Naomba niulize Wizara kupitia Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri pamoja na watendaji; changamoto ambazo hazikuweza kushughulikiwa katika kipindi cha mwaka 2022/2023, je, tutaweza kuzishughulikia changamoto hizo katika kipindi hiki cha 2023/2024?

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ni nyingi, moja ikiwa ni migogoro mikubwa ya ardhi inayolikumba Taifa letu. Nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweza kuweka nia ya dhati kabisa ya kuwasaidia wananchi wa nchi hii kupitia migogoro hii ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la Mradi wa KKK, Wizara imeweza kutoa fedha za mikopo katika halmashauri mbalimbali, lakini kuna halmashauri ambazo zimeweza kufanya vizuri na kuweza kukusanya mapato na kurudisha mikopo hiyo. Hata hivyo, zipo halmashauri kadhaa ambazo zimeweza kuchukua mikopo lakini hazikuweza kurejesha mikopo hadi hivi sasa, lakini pia wanaendelea kutekeleza miradi mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zile zinatakiwa zirejeshwe ili baadaye halmashauri nyingine ziweze kutumia fedha hizo ambazo zinasubiri. Hiyo ni changamoto kubwa ambayo Wizara wanatakiwa kutuhakikishia kwamba fedha hizi zinarejeshwa haraka ili ziweze kuwasaidia halmashauri nyingine ambazo zinasubiri fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la migogoro ya ardhi; migogoro hii kama walivyosema Waheshimiwa wenzangu, ni mikubwa na ni mingi sana. Kwanza, niipongeze Wizara kwa kuweza kupata Shilingi Bilioni 350 ambazo ni sawa na Dola za Kimarekani milioni 150 ambazo zitaweza kusaidia kwa kiwango kikubwa kuondoshwa migogoro hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kusikitisha ni kwamba Wizara katika mradi huu imeweza kujielekeza katika halmashauri 41 tu katika kutatua na kutekeleza miradi hii ambayo ni pamoja na kupanga na kupima katika maeneo ya halmashauri hizo. Migogoro ya ardhi iko nchi nzima, kwa nini Wizara ijielekeze katika halmashauri 41 tu? Katika halmashauri hizo 41 katika fedha hizi imejipangia kutatua migogoro ya ardhi, kwa kushughulikia vijiji 500 tu ambavyo kila mwaka watakuwa wanashughulikia vijiji 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini, kwa vile tunayo Tume yetu ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi na ina ukwasi mkubwa katika kupata fedha za kuendeleza miradi ya maendeleo ambao ni ule Mradi wa Kupanga na Kupima Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Wizara isitenge bilioni 62 tukafuata maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu ambayo imeelekeza mpaka ifikapo mwaka 2025 vijiji vipya 4,131 viwe tayari vimeshapimwa. Kwa nini Wizara kupitia fedha hizi tusitenge shilingi bilioni 62, tukazielekeza katika tume hii na kuanza kutekeleza Mradi huu wa KKK katika vijiji vyote na tukahakikisha kwamba mwaka 2025 vijiji vyote viwe tayari vimeshapimwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, 2025 haiko mbali, Chama Cha Mapinduzi kiliingia mkataba na wananchi na kikawahakikishia kwamba ifikapo mwaka 2025 vijiji vyote vitakuwa vimepimwa. Kwa nini tusitenge fedha, shilingi bilioni 62, tukaenda tukatatua migogoro ya ardhi kwa kuangalia suala la kupanga na tukaweza kupata mapato makubwa kupitia mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana, Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote tukae tuupitie tena mradi, tuangalie namna ya kutenga shilingi bilioni 62 ili tuzielekeze katika mradi huu wa kupanga ili kuhakikisha kwamba tumekwenda na maelekezo ya Ilani, ifikapo mwaka 2025 vijiji vyote 4,131 viwe tayari vimeshapimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna jumla ya vijiji 12,318, lakini vijiji vilivyopimwa ni 2,818 tu ambayo ni sawa na asilimia 23. Tutakapoingia katika mradi huo na kuweza kutenga fedha ya kutosha tutaweza kupima vijiji 826 kila mwaka. Tutaweza kuondosha migogoro ya ardhi kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kuhusu asilimia 30 ya mapato ya halmashauri ambayo fedha hizi zilikuwa zinabaki ndani ya halmashauri na kuweza kuwanufaisha na kuweza kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi halmashauri husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha, karibuni tu tutakuwa na bajeti hapa na kupitia sheria mbalimbali, naomba sana Serikali tuweze kurekebisha sheria hii na kuelekea kwenye kanuni na miongozo mbalimbali ili fedha hizi asilimia 30 ziendelee kubaki halmashauri ili ziendelee kuzisaidia halmashauri katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niunge mkono taarifa ya Kamati, lakini pia niendelee kuunga mkono hoja ya Wizara lakini kwa kuona kwamba changamoto zote ambazo tumezieleza, ziweza kufanyiwa kazi, ahsante.. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na afya njema na hadi kuweza kusimama katika Bunge hili tukufu jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya katika Taifa letu na kuimarisha majeshi yetu haya kuhakikisha kwamba changamoto wanazokabiliana nazo zimeondoka ili kuimarisha suala la amani na utulivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote, lakini pia niwapongeze majeshi yetu yote nchini kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha kwamba usalama wa raia pamoja na mali zao umepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika Jeshi letu la Polisi lakini kupitia ufinyu wa bajeti, wastaafu wa Jeshi la Polisi, pamoja na mifumo ya kumbukumbu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jeshi letu hili tunatambua kwamba limekuwa likifanya kazi kubwa na ya mfano katika Taifa letu na wanafanya kazi usiku na mchana, lakini la kusikitisha wana changamoto kubwa kutokana na ufinyu wa bajeti katika utekelezaji wa majukumu yao. Kitengo cha mafuta kinasuasua, mishahara yao inasuasua, magari mabovu, ofisi hazijulikani, vifaa vya ofisi havijulikani. Tumekuwa tukipitisha bajeti hapa na kuona kwamba angalau kutakuwa na unafuu katika utekelezaji wa majukumu yao katika utekelezaji wa bajeti hiyo, lakini baada ya bajeti ile kupitishwa tu changamoto zile zinaendelea kuwepo siku hadi siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matumaini yetu kwamba katika bajeti hii ambayo Mheshimiwa Waziri ameiwasilisha hapa, taarifa ya bajeti ni nzuri, imepangika vizuri, ni mategemeo yetu kwamba utekelezaji wa bajeti hii utaweza kwenda kulenga changamoto zote zile zinazowakabili jeshi hili katika maeneo yote Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Serikali kwa juhudi zake ambazo zinaongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya hadi kuhakikisha kwamba jeshi letu hili au majeshi yetu haya yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya Mkoa wa Kaskazini Pemba pamoja na changamoto hizo nilizozitaja, zipo changamoto kadhaa ambazo jeshi hili wamekuwa wakikabiliana nazo. Katika changamoto hizo moja ilikuwa ni magari, tunaishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mkoa wa Kaskazini Pemba tumeweza kupatiwa magari mawili. Gari moja liko pale Makao Makuu ya Mkoa, lakini gari lingine limeelekezwa katika Kituo cha Polisi Mchanga Mdogo. Wanafanya kazi kwa kuhudumia wananchi kama kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa ni mafuta, hawana mafuta ya kufanyia kazi, uchakavu wa ofisi pamoja na vifaa vya ofisi, lakini pia majengo chakavu. Majengo yote ya Mkoa wa Kaskazini baadhi tu lakini askari wengi wanakaa uraiani. Si vema Askari Polisi pamoja na kazi zao kukaa uraiani kwa sababu kuna kazi zingine wanazofanya wanarudi usiku lindoni na mambo mengine. Kwa hiyo ni vema tukakarabati zile ofisi hasa pale polisi line, kuna ofisi nzuri tu ambazo majengo yake tumeyarithi kwa kipindi kirefu, kwa hiyo ningeomba yafanyiwe ukarabati mkubwa kwa sababu majengo yale ni mazuri. Pale kuna Mesi na mambo mengine, huduma za afya na mambo mengine. Kwa hiyo yakikarabatiwa majengo yale na majengo mengine yaliyoko Michewene na vituo hasa kituo kingine Matangatuani na Konde kwa hiyo Mkoa wa Kaskazini Pemba tutakuwa tumeondoa changamoto kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wastaafu. Kumekuwa na ukwasi mkubwa kuhusu suala la wastaafu wa Jeshi la Polisi. Mara nyingi unapotegemea kustaafu unategemea kwamba utapata haki ambayo itaweza kukusaidia katika maisha baada ya kustaafu. Askari wetu hawa wamekuwa wakidhalilika katika hali ya umaskini sana na wanaodhalilika sana ni kuanzia cheo cha Kuruta, Koplo, Sajenti, Senior Sajenti mpaka Inspector kidogo kumekuwa kama kuna makundi fulani kati ya huku na huku. Kwa hiyo ningeomba sana changamoto hii iweze kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kuna wastaafu ambao wameshalipwa haki zao kupitia mafao yao ambayo PSSSF tayari wameshawalipa, lakini kuna fedha za kusafirisha mizigo pamoja na nauli. Malalamiko ni makubwa, askari ni wengi sana wanaodai hizo haki, ni wengi mno, sasa hivi wanadai haki zao za kusafirisha mizigo ambapo wengine walikuwa wanafanya kazi Morogoro, wengine walikuwa wanafanya kazi mikoa mingine tofauti tofauti, lakini fedha zao hawajalipwa. Kwa hiyo inasikitisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi juzi tu walipeleka malalamiko maeneo tofauti tofauti ikashindikana, wakapeleka malalamiko kwa Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, mmojawapo katika Wakuu wa Mikoa wangu waliopo, akawatishia kuwapeleka kwa Mheshimiwa Rais. Matokeo yake haki zile waliweza kupatiwa mara moja. Nauliza hizi fedha zilitoka wapi na katika bajeti gani? Walipolalamika tu na kutishiwa na Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, basi waliweza kulipwa hizi haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sasa hivi utaratibu uliopo jeshini ni kuwa, ndani ya miezi mitatu kabla ya kustaafu, watumishi hawa wanalipwa haki zao za kusafirisha mizigo pamoja na nauli, lakini wale waliostaafu kipindi cha mwaka 2020/2021, haki zao hadi leo hawajapewa. Kwa hiyo hao watawekwa katika bajeti ipi? Nauliza, haki zao zitaingizwa katika bajeti ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la mifumo ya kumbukumbu. Kumekuwa na ukwasi mkubwa katika mifumo ya kumbukumbu Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na watendaji wa Wizara tunaomba masuala ya kumbukumbu yaangaliwe upya katika jeshi hili kwa sababu kunakuwa na utofauti sana katika ulipaji wa haki, lakini pia katika suala zima la utekelezaji, yaani tunamfanya mpaka yule askari husika, aweze kutokuwa na imani na jeshi lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna askari naomba baadaye nimkabidhi Mheshimiwa Waziri. Askari huyu ambaye alikuwa anafanya kazi katika kituo cha Morogoro, alikuwa katika cheo cha Senior Sajenti. Askari huyu aliugua akiwa kazini, lakini pia pamoja na kuugua akiwa kazini, jeshi halikuangalia kuugua kwake wala namna ya kujua matibabu yake. Familia ikamsafirisha ikampeleka nyumbani Zanzibar, askari yule kwa bahati mbaya alifariki dunia, lakini alifariki dunia mwaka 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo mwaka mmoja baadaye inakuja barua ya kustaafu askari yule, pamoja na kupeleka vitambulisho na mambo mengine anaambiwa anastaafu kwa umri wa lazima wa miaka 55, lakini pia arejeshe vitambulisho pamoja na sare na mambo mengine, wakati askari yule ameshastaafu, mwaka mmoja baadaye ndio inakuja barua ya kustaafu, wakati amefariki.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Maida muda wako umekwisha.

MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja.