Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Julius Kalanga Laizer (2 total)

MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Waziri Mkuu swali:-

Mheshimiwa Waziri Mkuu, pamoja na mpango mzuri wa Serikali wa kuhakikisha kwamba, kila kijiji kinapelekewa umeme katika nchi yetu. na kwa kuwa, Serikali imejitahidi sana kupeleka nguzo nyingi na nyaya katika maeneo mengi ya nchi yetu, lakini bado nguzo hizo zimeendelea kulala chini na nyingine hazijafungiwa umeme. Na kwa kuwa mpango wa REA Awamu hii ya Tatu ni kwamba, lazima uishe mwezi wa sita, lakini katika mwenendo wa utekelezaji wa mradi wenyewe inaonekana mpaka mwezi wa sita kuna miradi ambayo itakuwa haijakamilika.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba, mradi huu wa utekelezaji wa REA katika vijiji vyetu unakamilika mwezi wa sita kama ambavyo Serikali ilipanga?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Julius Kalanga Laizer, Mbunge wa Monduli, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo miradi hii ya REA ambayo inapeleka umeme vijijini ambayo kwa kweli kazi zinaendelea vizuri. Tumeenda maeneo mengi; na sasa tumefikia zaidi ya asilimia 60 na kitu katika kuweka umeme kwenye vijiji vyetu vingi ambavyo vimekusudiwa. Mkakati huu unalenga kila kijiji huko kwenye maeneo yetu tunakotoka. Wizara ya Nishati imejipanga vizuri, imeshasambaza wakandarasi kila halmashauri, wakandarasi ambao wamesaini mkataba kukamilisha kazi hiyo kwa muda na kwa kuweka umeme katika kila kijiji kwa awamu hii ya tatu, awamu ya kwanza na kwenye awamu ya tatu kuna awamu ya kwanza na ya pili na zote hizi zitatekelezwa, ili kuhakikisha kwamba, umeme unapelekwa kwenye ngazi ya vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hiyo ambayo nimeeleza kwamba inaendelea na ni nzuri inaanza sasa kupeleka umeme kwenye vijiji vyetu vingi; na vijiji vyote vilivyobaki viendelee kuwa na uhakika kwamba, umeme utafikishwa. Sasa suala la kufika mwezi wa Juni inategemea hapa katikati kama kunaweza kuwa na jambo lolote lile linaloweza kumfanya mkandarasi akashindwa kukamilisha kazi yake vizuri. Sisi ndani ya Serikali tunahakikisha mtiririko wa fedha za malipo kwa mkandarasi unakwenda, tunahakikisha kwamba, vifaa anavipata.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa bahati nzuri sasa vifaa vya kutengenezea kazi hizo vinapatikana hapahapa nchini. Nguzo zinapatikana nchini, transformer zinapatikana hapa nchini, nyaya zinapatikana hapa nchini. Kwa hiyo tuna matumaini kwamba, tunaweza kukamilisha kazi hiyo kwa kipindi ambacho tunatarajia, na kwa kuwa, wakandarasi wako kazini na tumetoa pia mamlaka kwa TANESCO zetu maana TANESCO na REA ni taasisi mbili zilizo kwenye Wizara moja, ili TANESCO sasa wasimamie kazi za REA kuwa zinakamilika kwenye maeneo ambayo wanayasimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumini yangu kwamba kazi za uwekaji umeme kwenye vijiji itakamilika. Mheshimiwa Waziri wa Nishati ameelza hapa, kwamba sasa tunakwenda mbali zaidi mpaka kwenye vitongoji vikubwa navyo tunapeleka umeme. Kwa hiyo wananchi wawe na matumaini na wajiandae sasa kutumia fursa ya kuwa na umeme kwenye maeneo yao kwa ajili ya kuendesha shughuli mbalimbali zinazohitaji umeme, asante sana. (Makofi)
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimia Spika, nakushukuru. Mwaka huu maeneo mengi ya nchi yetu yamekabiliwa na upungufu wa mvua ambayo imepelekea maeneo mengi kukosa chakula cha uhakika na hivyo kusababisha bei ya chakula kupanda kwa kiasi kikubwa sana. Hapa tunapozungumza maeneo mengi mahindi yanauzwa kuanzia shilingi elfu 80 mpaka laki moja.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba chakula cha bei nafuu kutoka NFRA kinapelekwa katika maeneo haya yaliyokumbwa na ukame ili wananchi waweze kumudu chakula? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kalanga, Mbunge wa Monduli kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uzalishaji wa chakula nchini kwa maana usalama wa chakula nchini kufuatia msimu uliopita wa uvunaji wa mazoa ya chakula uko vizuri, lakini tunatambua kwamba yako maeneo kadhaa hali ya hewa haikuwa nzuri na uzalishaji wake haukuwa mzuri sana. Kwa hiyo, maeneo hayo yanaweza kuathirika kwa kuwa na bei zisizotabirika wakati wote na kusababisha wananchi kutojua hasa bei ya mahindi, chakula hicho, lakini pia ni wapi tunaweza kupata chakula hicho.

Mheshimiwa Spika, lakini nataka niwahakikishie kwamba uzalishaji wa chakula ambao umefanywa, ambao Wizara ya Kilimo imeweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba maeneo yote yanapata chakula, NFRA imepewa jukumu la kuhakikisha kwamba usalama wa chakula nchini unaimarishwa kwa kuwa na chakula cha akiba kwenye maghala ili kiweze kutolewa na kuuzwa kwenye maeneo ambayo hayana chakula kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili, kwa kuwa chakula kiko nchini na tunao wafanyabiashara ndani ya nchi, hiyo ni fusa muhimu kwao ya kupata chakula kukipeleka maeneo ambayo hayana chakula. Mheshimiwa Kalanga amezungumzia bei nafuu, bei nafuu sasa ni tumeruhusi wanunuzi mbalimbali kuingia kununua. Wanapokuwa wanunuzi wengi kunakuwa na ushindani wa ununuzi, ingawa pia bei inakuwa iko juu lakini sisi kwa sababu tuna NFRA ambayo inashughulikia usalama wa chakula, basi chakula huwa kinapatikana. Kwa hiyo, muhimu zaidi tupate taarifa, wapi kuna upungufu wa chakula, halafu tuone, tuweze kupeleka chakula ambacho tunaweza kununua kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, lakini muhimu zaidi ni ule msisitizo wa kila mmoja afanye kazi na tumeanza kuona matunda kwamba chakula sasa uzalishaji ni mkubwa mpaka tunakua na ziada hapa nchini na chakula kingine tunauza pia hata nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, lakini mbili, ni hilo ambalo tumelisema la kwamba wanunuzi sasa wapite maeneo hayo waweze kuchukua mahindi kutoka eneo moja kupeleka eneo la pili ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kupitia Mheshimiwa Kalanga NFRA inaweza ikipata taarifa na Wizara ya Kilimo inasikia hapa ni rahisi sasa kuweza kushughulikia maeneo hayo yanayokosa chakula. Kwa hiyo, kwa taarifa ambayo tumeipata sasa naamini tutaishughulikia ili kuona namna nzuri ya kufikisha chakula ambacho tunaweza kukinunua kwa bei nafuu. Ahsante.