Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kemirembe Rose Julius Lwota (8 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. KEMIREMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kukushukuru wewe kwa kuweza kunipa nafasi hii ya kuchangia, vilevile napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kunifikisha hapa siku hii ya leo na kuwashukuru wanawake wote wa Mwanza walionipigia kura kwa wingi kabisa nasema ahsanteni wote na ninawaahidi sitowaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda kushukuru na kumpongeza Rais wetu John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kufanya na hotuba nzuri sana aliyotufungulia Bunge letu hili.
Vilevile napenda kuwapongeza Mawaziri wote walioteuliwa na Mheshimiwa Magufuli, amewaamini na sisi wote tunawaaamini na tunaona kazi mnazozifanya na tunawapongeza tunasema kazeni buti tuko nyuma yenu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kuunga mkono asilimia mia moja hotuba ya Mheshimiwa Rais. Mambo aliyeyasema kwenye hotuba yake ni mengi yamehusisha nyanja zote, kwa Mtanzania na kwa maendeleo ya Tanzania yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameongelea suala la miundombinu, ameongelea suala la reli na suala barabara. Kwanza kabisa napenda kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri inayofanya kwenye barabara zetu, wote ni mashahidi, barabara zimeunganishwa, Mikoa tofauti mingi imeunganishwa kwa lami na wote tunafahamu. Mheshimiwa Rais alishawahi kutoa mfano humu Bungeni akasema barabara za lami zilizopo Tanzania zingekuwa Burundi wasingepata hata sehemu ya kulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo natoa pongezi sana kwa mambo yanayofanyika na Serikali yetu ya Cha cha Mapinduzi. Napenda nijikite kwenye suala la barabara baada ya mvua za elnino zilizoanza kunyesha hivi karibuni mwezi Novemba Mkoa wa Mwanza tulipata matatizo makubwa ya maafa, watu walipoteza maisha. Lakini vilevile barabara zetu zimeharibika sana kwa Majimbo yote mawili ya Mjini, nikiwa na maana ya Jimbo la Ilemela na Nyamagana.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya uharibifu huo, jitihada zilifanyika kwenye Halmashauri zetu, Halmashauri zikaandika barua TAMISEMI, TAMISEMI wakatuma wataalam wakaja Mkoa wa Mwanza, wakazunguka na ma-engineer wetu wa Wilaya zote mbili na wakaona uharibifu zaidi umefanyika kwenye Wilaya ya Ilemela.
Mheshimiwa Spika, utafiti huo ulifanyika mwezi Novemba na baada ya hapo mvua zimeendelea kunyesha sana, na mpaka hivi tunavyoongea mvua zinanyesha na barabara za Mwanza hususani Ilemela zimekatika kabisa. Baada ya wataalam hao kuja, walifanya emergence plan kana kwamba barabara za Mwanza hususani za Ilemela zitengewe fedha na zije zitnegenezwe, lakini mpaka sasa hivi ninavyoongea jambo hilo halijafanyika, barabara hizi ambazo zimekatika kabisa zinafanya wananchi wetu wanashindwa kufika mahali wanapotaka kwenda kwa wakati, gharama za usafiri kwa maeneo yanayopitika zimekua juu, akina Mama wajawazito wanashindwa kufika hospitali kwa wakati, wanajifungulia barabani, hali kwakweli ya barabara ni mbaya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya barabara ambazo zimeharibika sana naweza kuzitaja. Mojawapo ni barabara ya Kirumba – Mwaloni ambayo inaenda kwenye soko letu la samaki la kimataifa. Barabara hii inaingiza fedha nyingi sana kwenye Halmashauri ya Ilemela na Serikali kwa ujumla wake, lakini barabara hii sasa hivi imekatika kabisa, maroli na magari makubwa yanashindwa kupita. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna barabara ya Kiseke PPF; barabara ya Busweru - National na barabara ya Bwiru.Tunamuomba Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Miundombinu kama kuna uwezekano hili suala litatuliwe kwa sababu hali ni mbaya sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni Waziri alifika Mkoa wa Mwanza akatoa ahadi ya kujenga barabara ya lami inayotoka Sabasaba kwenda Busweru. Barabara hiyo hali ni mbaya na safari hii mpaka barabara imefungwa yaani haitumiki tena, kwa hiyo, tunaomba kwenye bajeti hii inayokuja tutengewe hizo fedha za huu mradi ambao Mheshimiwa Waziri ametupa ahadi na utekelezwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kuchangia kwenye masuala ya afya, wote ni mashahidi masuala ya afya wote ni mashahidi hotuba ya Mheshimiwa Rais, aliongolea suala la afya kwenye kurasa za mbele kabisa za hotuba yake na wote ni mashahidi tumemwona baada ya kuapishwa siku chache ya sehemu ambazo amezitembelea ni Muhimbili na amejionea changamoto zilizopo kwenye hospitali zetu za Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto zilizopo Muhimbili hazina tofauti sana na changamoto zilizopo Mkoani kwetu Mwanza. Tuna hospitali ya referral ya Sekou Toure. Hospitali hii inahudumia watu wengi sana na inatoa huduma nzuri sana na ndiyo maana nadhani watu wanakuwa wengi na wazee, akina mama na watoto wanahudumiwa bure. Napenda kupongeza Serikali kwa jitihada hizi wanazozifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini changamoto bado ni nyingi vilevile hapo tulipo. Moja ni ufinyu wa bajeti, bajeti inayotakiwa kwenda kwenye hospitali yetu ya Sekou Toure haiendi kwa wakati na ikienda haiendi bajeti kamili. Najua Waziri na Naibu Waziri sasa hivi tumepata ni wachapakazi na nina imani haya mambo tunayoongea hapa yatatekelezeka.
Mheshimiwa naibu Spika, kuna suala la vifaa tiba. Changamoto za vifaa tiba pia ni nyingi pale, hospitali inahudumia watu wengi x-ray iliyopo ni moja na ni x-ray ambayo imekuwepo tangu hiyo hospitali inaanzishwa. Kwa hiyo tunaomba Mheshimiwa Waziri utusaidie kwa hilo, ni hospitali ambayo inahudumia wakazi wengi sana wa Mwanza na mikoa ya jirani.
Mheshimiwa Spika, suala lingine nilitaka kuongelea ni kuhusu afya ni kuhusu hospitali ya Wilaya ya Ilemela. Hospitali hii tunashukuru sana Serikali kwa sababu inaendelea vizuri, imeshapewa hela almost 80 percent ya kazi zinazotakiwa kufanya, kwa hiyo iliyobaki ili hospitali ikamilike tuweze kupata hospitali ya Wilaya ya Ilemela ni fedha ndogo sana. Tunaomba Mheshimiwa Waziri tunapokuja kujadili bajeti utusaidie kutenga hela za hospitali ya Wilaya ya Ilemela. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna kituo cha afya cha Buzuruga. Kituo hiki cha afya kinahudumia wakazi wengi sana wa Mwanza kwa sababu kwa upande wa Ilemela hatuna hospitali ya Wilaya, kwa hiyo watu wengi sana wanajikuta wanaenda kwenye hicho kituo cha afya lakini kituo cha afya hiki pia kina changamoto na hatuna wodi ya wanaume. Kwa hiyo, wanaume wanapokuja kuhudumiwa pale hata kama wanaumwa kiasi gani cha kuwa admitted hawawezi kuwa admitted kwa sababu hatuna wodi, kwa hiyo tunaomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hili na kutupa kipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la watoto njiti. Suala hili ni changamoto, watoto hawa kwenye hospitali zetu nyingi kwa Mkoa wa Mwanza hawana wodi za watoto njiti, wodi hazipo watoto hawa wakitokea wamepatikana na matatizo hayo wanachanganywa na wodi za kawaida, yaani katika wanawake waliojifungua kawaida watoto, suala hili ni nyeti sana naomba Mheshimiwa Waziri tuliangalie.
Vilevile vifaa vya kuhudumia watoto hawa kama incubators, suction machines, feeding tubes, ni vitu ambavyo gharama yake siyo kubwa sana lakini vinakosekana kwenye hospitali zetu.
Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri tunakuomba utuangalie kwenye hilo suala la watoto njiti na pia kama kuna uwezekano research ifanyike, tujue hawa watoto wapo kiasi gani na wanapatikana sana kwenye Wilaya gani ya Tanzania ili tuweze kufanya utafiti na kujua ni kitu gani kinapelekea watoto hao wanakuwa njiti.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Afya. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu. Napenda vilevile kuwapongeza Mawaziri wetu kwa kazi nzuri wanayoendelea kufanya na nataka tu kuwapa moyo wazidi kufanya kazi, Wizara hii changamoto ni nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuwapongeza watumishi wetu wa afya. Kwa kweli wanafanya kazi ngumu kwenye mazingira magumu, hospitali zetu nyingi hazina vifaa tiba, hazina dawa, hazina vitendea kazi na bado wanapata lawama nyingi kutoka kwa wananchi kitu ambacho kwa kweli si sawa. Nadhani kama Wabunge na wananchi tungejitahidi kuwapa moyo waendelee kufanya kazi kwa bidii katika mazingira hayo na tuwape moyo kwamba Serikali ya sasa hivi ya Awamu ya Tano ipo makini na changamoto zote zitatatuliwa, ni suala la muda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji wengi wamechangia suala la vifo vya akinamama na takwimu zimeonyesha wanawake 42 wanakufa kila siku. Hili ni suala la kushtua na inabidi lifanyiwe kazi haraka iwezekanavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine la hospitali na vituo vyetu vya afya. Unakwenda kwenye vituo vya afya unakuta hakuna maji na umeme. Inafika mahali kuna watu wanaogopa kwenda hospitali kwa sababu anajua akienda hospitali atatoka na magonjwa mengine ambayo yanaambukizwa kutokana na mazingira mabovu ya hospitali zetu. Suala la maji na umeme kwenye hospitali zetu ni mambo muhimu kabisa ambayo inabidi yaanze kufanyiwa kazi kwenye hivi vituo ambavyo viko tayari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuchangia ni kuhusu population growth, ongezeko la watu hasa nchini kwetu. Tatizo hili ni kubwa, ni changamoto kwetu na nashangaa ni kwa nini watu wengi hawaliongelei suala hili. Tutakaa hapa tutaongelea suala la umaskini lakini ni vigumu sana kwa rate ya ukuaji wetu wa asilimia 2.7 tukatoka kwenye hali hii tuliyopo, ukuaji wetu ni mkubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano mdogo tu wa mwaka 1961 wakati tunapata uhuru nchi yetu ilikuwa ina watu milioni tisa, nchi kama Norway walikuwa na watu milioni 3.6, leo hii sisi tuna watu karibia milioni 50, nchi ya Norway ina watu milioni 5.6. Kwa hiyo, tukiendelea kuongelea suala la shule za kata itaendelea kuwa changamoto kama rate ya kuongezeka inazidi kukua kwa kiasi hiki, changamoto hizi ni vigumu sana kwisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara ya Afya tujitahidi kuelekeza nguvu kwenye uzazi wa mpango (family planning). Hili siyo kwa Wizara tu, nadhani ni changamoto yetu sote na bila kujali vyama wala itikadi zetu, tunapokwenda majimboni, tunapofanya mikutano yetu tuongelee suala la uzazi wa mpango. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uzazi wa mpango ni changamoto na inabidi tulizungumzie watu wajue. Kuna maeneo unakwenda, mfano Mwanza huko kwetu, unaongea na akinamama hawajui haya mambo, hawajui kama kuna contraceptive pills, hawajui kama kuna njia za kuweza kutumia ili usipate watoto wengi, anakwambia mimi nitazaa mpaka watakapokwisha, sasa wataishia wangapi? Kwa hiyo, nadhani hili suala tungelipa kipaumbele kama tunavyofanya upande wa diabetes, ugonjwa wa moyo, cancer, family planning pia iwe priority. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine baadhi ya wachangiaji wameliongelea nami naomba nitoe msisitizo kidogo kwenye hilo, ni suala la afya ya akili (mental illness). Hili suala ni changamoto na kwa nchi yetu nadhani ni kitu ambacho kimekuwa kama ni aibu, hakitakiwi kuongelewa na mtu akionekana ni mgonjwa inakuwa kama ni laana au umerogwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tunatakiwa kuwa na uelewa na kampeni ifanyike kuhusu hili suala la ugonjwa wa akili. Nchi zilizoendelea tafiti zimefanyika, nchi kama Marekani wanasema kila watu watano kuna mtu mmoja ambaye ni mgonjwa wa akili. Nchi kama Uingereza wamefanya research wanasema kila walipo watu wanne mmoja ana ugonjwa wa akili. Nchi kama Australia vilevile wamefanya utafiti wanasema kila walipo watu watano mtu mmoja ana ugonjwa wa akili. Hili suala siyo la kulifumbia macho na inabidi tusiwe na aibu tuliongelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na research ya WHO ya mwaka 2014 inasema, 25% of the population worldwide will suffer mental illness. Around four hundred and fifty million people currently suffer from such condition, placing mental disorder among the leading causes of ill-health and disability worldwide. Nina imani kabisa hata hapa kwetu ikifanyika assessment, ukifanyika utafiti wagonjwa ni wengi na siyo suala la kulifumbia macho. Tusione aibu majimboni kwetu na kwenye familia zetu kuliongelea suala hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala lipo na mmoja wetu hapa anaweza akaugua, ni vitu vya kawaida kabisa na wanasema, there is no physical health without mental health likewise there is no mental illness without physical health. Kwa hiyo, hivi vitu vinakwenda pamoja. Naomba tusichukulie hiki kitu kama ni mzaha kwa sababu ni kitu ambacho ni serious kabisa na tukiongelee na ikiwezekana kama kuna uwezekano tutafute Madaktari waje watupime hata humu ndani ni kitu muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka kuongelea kuhusu suala la damu. Suala la damu ni janga la Kitaifa. Kule kwetu Mwanza kuna watu wanakufa, wajawazito wanakufa, watu wanapata ajali wanatakiwa kuongezewa damu lakini damu safi na salama haipo. Hili suala ni jukumu letu sote siyo la Serikali peke yake, tuhamasishe watu, sisi pia wenyewe kama kuna uwezekano twende tujitolee damu. Leo linaweza likampata mtu mwingine lakini kesho na kesho kutwa inaweza ikawa miongoni mwetu au miongoni mwa familia zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili suala ni la kuhamasishana, damu ni ya muhimu sana na upungufu wa damu upo na siyo tu Dodoma. Kwanza napenda kumpongeza Makamu wa Rais, mwanamke mwenzetu juzi amejitokeza akatoa damu na akahamasisha, hili jambo inabidi tulifanye sisi sote kwa sababu linahusu watu wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. KEMIREMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya kwanza ya Serikali hii ya Awamu ya Tano.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kuipongeza Serikali kwa jitihada na uthubutu iliyoweza kufanya na kutenga asilimia 40 ya fedha za bajeti yote kwenda kwenye mfuko wa maendeleo. Fedha hizi zilizotengwa za kwenda kwenye mfuko wa maendeleo ni nyingi na ni mara ya kwanza, haijawahi kutengwa fedha nyingi kiasi hicho kwenda kwenye mfuko huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni jukumu na rai yangu kwa Watanzania wote kum-support Mheshimwa Rais kwa kukusanya mapato, kuyatunza na kuyatumikia vyema haya mapato yetu ambayo tutakuwa tumeyapata ili tuweze kufikia dhamira yetu ya Serikali ya Awamu ya Tano.
Mheshimiwa Naibu Spika, maendeleo ni ya Watanzania wote kwa ujumla, hayachagui Chama wala itikadi. Kwa hiyo, ni rai yangu kwamba wote tuwe kitu kimoja ili haya mambo tuweze kuyafanikisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie kwenye suala la utalii, wenzangu wengi wamelizungumzia hili suala nami naomba nilichangie. Suala la kuongeza kodi kwenye utalii ni janga la kitaifa na Waheshimiwa Wabunge tukiliunga mkono hili tunavunja kabisa utalii wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kodi inayowekwa kwenye utalii ukilinganisha na nchi nyingine za jirani kwa mfano Kenya ambao ndio competitives wetu wakubwa kwenye masuala ya utalii, bajeti yao ya mwaka huu peke yake wametenga fedha za Kenya zaidi ya bilioni 4.5 ambayo ni sawa na shilingi bilioni 90 za Kitanzania, kwenye utalii pekee. Sisi bajeti yetu ni takribani bilioni 135, kwenye Utalii na Maliasili. Kwa hiyo, bado changamoto ni kubwa sana kwenye suala hili la utalii kwa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la utalii tumeweka kwenye mpango wetu wa mwaka huu kwamba tunaweka target ya kufikisha watalii 2,000,000 kwa mwaka. Watalii hawa kwa vigezo hivi vinavyowekwa vya kuongeza kodi, dhamira hii ya kufikisha watalii 2,000,000 itakuwa ni ndoto, haitawezekana. Watalii hawa hawatakuja kwa sababu ya ongezeko la kodi kwenye utalii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiachilia hapo, Tanzania, ni moja ya one of the expensive destination in East Africa kwa utalii. Kwa hiyo, kwa kuongeza hili, tunafanya gharama ziwe maradufu kwa sababu ya kodi hizi. Vile vile katika suala la utalii siyo kitu cha kujaribisha; tumetumia muda mwingi na gharama kubwa kuweza kufikisha watalii ambao tuko nao sasa hivi. Mwaka 2016 tumekuwa na watalii zaidi ya milioni 1.1 na target yetu kama nilivyosema ya 2,000,000 tukishaanza kuweka haya mambo ya kodi tutafanya watalii wetu wakimbie na wasije tena Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nataka kuongelea suala la kilimo. Kuna changamoto nyingi sana kwenye kilimo na napenda kuipongeza Serikali kwa kuweza kutoa kodi kwenye mazao ya kilimo, kwa mfano, maharage ya soya na mbogamboga. Ili kukamilisha sera ya viwanda ambapo tunataka uchumi wetu uwe wa viwanda, asilimia 65 ya kilimo inategemewa kwenye kuendeleza viwanda vyetu nchini. Kwa sababu hizo, kwenye bajeti nzima hakuna sehemu yoyote ambayo inaongelea investment kwenye kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kitabu cha Mpango wa Bajeti 2016, Mheshimiwa Waziri wa Fedha, amezungumzia suala la kilimo cha umwagiliaji, lakini kwenye bajeti halisi ya mwaka huu hakuna fedha yoyote ambayo imetengwa kwenye kilimo cha umwagiliaji. Tukitaka kuendeleza kilimo chetu, hatuwezi kutegemea kwenye kilimo cha msimu wa mvua peke yake, inabidi ifike mahali tuwekeze kwenye kilimo cha umwagiliaji kama tunataka kufanikisha Serikali ya viwanda na kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo kubwa sana la kilimo cha umwagiliaji. Asilimia 70 ya Watanzania ni wakulima na asilimia 23 ya pato la Serikali linatokana na kilimo, lakini hakuna investment yoyote ambayo imefanyika hapa pamoja na kwamba kuna maelezo tu ya kusema umwagiliaji utafanyika, lakini hamna suala lolote ambalo linazungumzia umwagiliaji. Umwagiliaji ni asilimia 10 tu ya hawa wakulima wote zaidi ya asilimia 70. Kwa hiyo, inabidi tujikite zaidi kwenye miundombinu na kuwawezesha wakulima waweze kulima kwa kilimo cha kisasa cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala la kuondoa kodi kwenye mazao ya maharage na mbogomboga; misamaha hii inalenga usalama wa chakula na siyo zaidi ya hapo. Misamaha hii ingeweza kusaidia na kuwa na tija kwenye uchumi wetu kama tungewekeza kwenye viwanda vidogo vidogo vya usindikaji. Tungewapa wasindikaji wa mbogamboga hizi na maharage waweze kufungua viwanda vidogo vidogo ambavyo vingeweza kusaidia kwenye ajira na vile vile kuongeza thamani ya mazao yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza uamuzi wa kuinua viwanda vidogo vidogo na usindikaji wa mazao ya mbogamboga kwa kutangaza misamaha ya kodi na ongezeko la thamani kwenye bidhaa zitokanazo na usindikwaji na ukuaji wa viwanda vidogo vidogo.
Vile vile, napenda kuipongeza Serikali kwa juhudi zake na kuweza kutenga fedha za kutengeneza reli ya kati ambayo imekuwa ni mazungumzo ya muda mrefu; wananchi wa Mkoa wa Mwanza wamekaa na wamesafiri na mabehewa haya ambayo yamekuwa mabovu kwa muda mrefu. Natoa pongezi sana kwa Serikali kwa kuamua kulifanya hilo na kununua meli ya Ziwa Victoria ambayo pia itaweza kusaidia wananchi wa Tanzania hasa ukanda wa Ziwa, Mwanza pamoja na Kagera. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna hili suala la CAG kuongezewa fedha. Suala hili limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi na naomba kutia msisitizo, suala la CAG kukatiwa fedha na fedha nyingi kupelekwa TAKUKURU, sidhani kama ni sawa, kwa sababu bila kuwepo huyu CAG, TAKUKURU hawatakuwa na kazi ya kufanya. Mambo mengi yanaibuliwa huko kwa CAG na baada ya hapo ndipo TAKUKURU wanaweza kupata mashiko na meno ya kufanya kazi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba hili suala liangaliwe na fedha kama inawezekana iongezwe kwa CAG ili aweze kufanya mahesabu yake na ukaguzi wake na kutuletea ripoti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kukushukuru kwa kuweza kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa kabisa anayoifanya na Watanzania wote wanaona, ninampongeza Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri wote kwa kazi kubwa wanazofanya na niwatie moyo ninawaambia wakaze buti, wapige kazi, hapa kazi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwapongeza pia Mawaziri Dada yangu Mheshimiwa Ummy na Naibu wake Mheshimiwa Kigwangalla kwa kazi kubwa wanazofanya, wametuletea ambulance kwenye Mkoa wetu wa Mwanza, wametupatia fedha za dawa, lakini hizi fedha za dawa mlizotupatia ni fedha ndogo hazitoshi, bado kuna baadhi ya vituo vyetu vya afya vina upungufu wa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kuzungumzia ni suala la vifo vya akina mama na watoto. Hili ni janga na naomba kama Serikali tulichukulie kwa umuhimu wake na tulipe kipaumbele. Kila siku ya Mungu akina mama kati ya 24 mpaka 30 wanapoteza maisha yao kutokana na uzazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watoto kati ya 170 mpaka 180 kila siku ya Mungu wanapoteza maisha kwa sababu ya vifo vitokanavyo na uzazi. Ninashukuru katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumza na amesema tukimpitishia bajeti hii itakuwa ni muarobaini wa haya masuala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa takwimu, mwaka 2000 kwa kila vizazi hai 100,000 vizazi 529 vilikuwa vinapotea, mwaka 2005 kwa kila vizazi 100,000 vizazi 578 vilikuwa vinapotea, mwaka 2010 vikapungua vikafika 454 na sasa kwa bahati mbaya mwaka 2015/2016 vizazi hivi vimeongezeka kwa kila vizazi 100,000 tunapoteza watu 556, hili ni janga na ninaomba sana Mheshimiwa dada yangu Ummy tulifanyie kazi hili ili tuweze kuepusha vifo hivi, akina mama hawa wakiwa wanatimiza wajibu wao wa msingi kabisa wa kupata watoto, kwa bahati mbaya vifo hivi vinatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vifo vingi vya akina mama hawa vinatokana na mambo makuu manne, jambo la kwanza ni upungufu wa damu, damu salama ya kuongeza akina mama hawa inakosekana akina mama hawa wanapoteza maisha. (Makofi)

Jambo la pili ni uzazi pingamizi, akina mama hawa wanapotakiwa kwenda kufanyiwa upasuaji zahanati wakati mwingine ziko mbali, zilizopo karibu hazitoi huduma ya kupasua akina mama hawa wanapoteza maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kifafa cha mimba, Mheshimiwa Ummy ameongelea na tiba ni sindano za magnesium sulphate. Ninaomba sana katika vituo vyetu vya afya mambo haya yawepo ili tuweze kuokoa vifo vya akina mama. Mimba za utotoni na kuharibika kwa mimba, akina mama hawa mimba zinaharibika wanaenda kwenye zahanati zetu hatuna vifaa vya kusafisha hizi mimba na hii inasababisha vifo kwa akina mama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la upungufu wa wataalam kwenye sekta ya afya, Mheshimiwa Waziri amesema kuna ajira mpya kwenye sekta ya afya lakini ni janga kubwa kweli, hatuna wafanyakazi wa afya wa kutosha. Naomba hili suala tuliangalie na tuajiri wafanyakazi wa afya ili tuweze kuokoa maisha ya Watanzania hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilisimama hapa na nikaongelea suala la vifaatiba. Hospitali yetu ya Sekou Toure kubwa kabisa ya Mkoa wa Mwanza hatuna CT Scan, tumeomba hapa Mheshimiwa Waziri akaahidi akasema CT Scan hii inakuja lakini mpaka sasa ninavyosimama na kuongea hapa CT Scan haipo. Hii inapelekea Watanzania wa Mkoa wa Mwanza waende kufanya vipimo hivi kwenye private clinics. Private clinics vipimo hivi ni kati ya shilingi 300,000 mpaka 400,000, ni aghali na Watanzania wengi hawawezi kumudu fedha hizi kuzilipa.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunaomba unapokuja hapa kuhitimisha utuambie ni lini vifaatiba hivi vitaenda kwenye Hospitali yetu ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la watoto njiti sijaliona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Watoto wanaozaliwa njiti ni wengi katika wodi yao, nimetembelea wodi yao Mkoa wa Mwanza, wodi haina vifaa. Watoto njiti hawa wanahitaji suction machines, wanahitaji blood pressure monitors, wanahitaji incubators ili waweze kuwekwa na kuhifadhiwa ili waweze kufika siku zao za kuweza kuruhusiwa na kwenda nyumbani, lakini inabidi watoto hawa waruhusiwe kwa sababu wodi ya watoto hawa haina vifaa. Mheshimiwa Waziri tunaomba sana uweze kutupatia vifaa hivi, wananchi na akina mama hawa wanahangaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la D by D, concept yake ni nzuri kabisa haina tatizo, lakini inatokea mkanganyiko kati ya Wizara ya Afya na TAMISEMI. Naomba ifike mahali sasa Wizara ya Afya isimame kama Wizara ya Afya. Tunapokuwa kwenye Halmashauri zetu huko tunauliza hili suala la afya mbona halifanyiki, mbona haliendi, tunaambiwa hili suala lipo TAMISEMI, ukienda TAMISEMI unauliza unaambiwa hili suala lipo Wizara ya Afya, sasa tufike mahali tuone ownership iko wapi na tujue Wizara ya Afya isimame kama Wizara ya Afya na tu-deal na Wizara ya Afya, peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba hii tumeona fedha zilizotengwa za dawa ni zaidi ya shilingi bilioni 230, kiuhalisia fedha za dawa zilizoenda ni shilingi bilioni 88 tu, nyingine zinaenda kwenye kusafirisha dawa, kwenye kujenga majengo, kwenye vifungashio, tungejua kabisa specific hela za dawa zimetumika...(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana kwa mchango wako.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA - MAKAMU MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA ARDHI, MALIASILI NA UTALII:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuweza kunipa nafasi ya kuja kuhitimisha hoja yetu ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kuwashukuru Wabunge wote kwa kuweza kutusikiliza na nina imani Wabunge wote mmeunga mkono hoja zetu za Kamati, na pia niwashukuru sana Wabunge wote waliochangia, kwa sababu ya muda sitataja Wabunge wote, ila nitataja tu idadi. Wachangiaji waliochangia kwa maandishi ni Wabunge 17 na wachangiaji waliochangia kwa kuzungumza Bungeni ni Wabunge 13.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiongelea suala la Wizara ya Ardhi, nadhani Mheshimiwa Waziri ameongelea na amejibu hoja nyingi za Waheshimiwa Wabunge na mapendekezo pia ya Kamati ameyaafiki, kitu ambacho pia sisi tunaunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho tunasisitiza kama Kamati ni Serikali itenge fedha za kutosha ili mambo yote, na mipango yote mizuri ambayo Wizara ya Ardhi inayo ya upimaji na urasimishaji wa ardhi nchini kote ufanyike ili kuweza kupunguza au kumaliza kabisa migogoro ya ardhi ambayo inaendelea sehemu tofauti tofauti katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Wizara ya Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Waziri, amejibu lakini hajajibu hoja za Kamati kama tulivyopendekeza. Lakini tushukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi anazoendelea kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo kadhaa kwenye Kamati tuliyaona na ni vema nikayasemea hapa pia. Sheria Namba 5 ya Wanyamapori ya mwaka 2009 imeainisha baada ya Sheria hiyo kuanza kutumika mwaka 2009, ilikuwa ndani ya miezi 12 itangaze upya mapori tengefu, maeneo oevu na hifadhi zote za Taifa, hii ilikuwa mwaka 2009.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni masikitiko kwa Kamati kwa sababu mpaka hivi leo tunaongea mwaka 2018, hii kazi haijafanyika na kufanyika kwa kazi hii kungeweza kusaidia mambo mengi sana ambayo yanaendelea hivi sasa. Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri wakati anachangia amekiri kuwepo vijiji ndani ya Hifadhi, hili suala lipo na kwa kweli tungeiomba Serikali itenge fedha ili hili suala liweze kumalizika na jinsi inavyoendelea kuliacha ndivyo linavyoendelea kuwa kubwa. Hii kazi ingefanyika mwaka 2009 ingekuwa tofauti sana na kama itakapokufa kufanyika mwaka 2018/2019 au 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na Wajumbe wengi wamechangia suala la migogoro ya mifadhi na wafugaji. Hili suala ni kubwa na karibia kila Mjumbe aliyezungumza na aliyeandika kwa maandishi wote wameliongelea hili suala, sasa tunaiomba Serikali hili suala likamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mheshimiwa Yussuf ameongelea suala la ushirikishwaji, sisi kama Kamati pia tuliliona ni vyema Serikali inapotaka kufanya jambo ishirikishe wananchi, ishirikishe wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kwamba Serikali ikitaka kufanya jambo lake bila kushirikisha wananchi na wawekezaji linaweza likakwamba. Vilevile mwekezaji akitaka kufanya jambo lake bila kushirikisha wananchi na Serikali ni dhahiri litakwama. Kwa hiyo, ni vema huu mtiririko huu ukafatwa na ukawa unafanyika ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala limeongelewa la uharibifu wa misitu, sisi kama Kamati pia tumeliona. Uharibifu wa misitu ni mkubwa sana unaoendelea nchini kwetu na hii yote inasababishwa na kazi na shughuli za kibinadamu, kuna ukataji miti hovyo ambayo miti tunayokata na tunayopanda ni vitu viwili tofauti kabisa.

Kwa hiyo, kama Kamati tunaishauri Serikali, kwanza kabisa ni kuelimisha hawa wananchi umuhimu wa kupanda miti na vilevile kuna suala la kuchoma mkaa, hili suala ni kubwa. Watanzania zaidi ya 80% wanatumia mkaa majumbani kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuweza kulisaidia hili suala na kuokoa miti yetu, ni vema Serikali ikaja na mkakati na mpango mzuri wa nishati mbadala na kupunguza gharama ili wananchi waweze ku-afford. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeongelea pia suala la kuweka alama kwenye hifadhi, ili pia ni suala ambalo linatakiwa kufanyika mapema. Tumeona kuna matatizo kwenye shoroba, lakini kwa sababu hakuna mipaka na wala hakuna Sheria ya maeneo haya. Kwa hiyo, ni vema Serikali ikajipanga na kuja na huo mkakati na ukafanyika haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imeongelea suala la Utalii ambao Mheshimiwa Waziri naye amelijibu, ni dhahiri kwamba Serikali yetu inapata mapato ya Taifa takribani 17.5% na vilevile fedha za kigeni kwa 12%. Kama Kamati tunataka tukushauri na kusema Wizara hii ni zaidi ya kidiplomasia, mahusiano ya nchi na nchi yanatakiwa. Tumeona forex hii inakuja kutokana na wageni wanaotoka nje. Kwa hiyo, kama Kamati tunaomba na tunaitaka Serikali kama inawezekana iweze kuwa na mahusiano mazuri na watalii vilevile na wawekezaji nchini kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kuunda Kamati Ndogo kama Kamati pia tulilipendekeza na napenda kulisisitizia. Mheshimiwa Lukuvi amejibu, amesema Kamati Ndogo ilifanyika na kina Lembeli na ndiyo inafanyiwa kazi mpaka leo, lakini sisi kama Kamati hatujawahi kuona majibu hayo. Kwa hiyo, kwa sababu hatujawahi kuyaona tumeona kama Kamati yetu sisi ni vema pia ikaifanya hii kazi upya na tukaja na mapendekezo hapa Bungeni na tukaona tunaanzia wapi kutokea hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa naliomba Bunge lipokee na kukubali taarifa ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa mwaka 2017 pamoja na maoni na mapendekezo yaliyomo katika taarifa hii.

Waheshimiwa Wabunge, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kuweza kunipa nafasi ya kuzungumza asubuhi hii ya leo. Vile vile niungane na Wabunge wenzangu wote na Watanzania kwa ujumla kwa kukukaribisha tena kwenye Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na Timu yake yote kwa hotuba zao nzuri ambazo wametuletea; vile vile nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ziara ambayo alifanya katika Mkoa wetu wa Mwanza, ziara ambayo imekuwa na mafanikio makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, sitatenda haki kama nitasimama kuchangia hapa leo nisiongelee masuala ya uvuvi ambayo yanaendelea kwenye Mkoa wetu wa Mwanza na Kanda ya Ziwa kwa ujumla wake. Kumekuwa na tatizo kubwa sana la unyanyasaji wa wavuvi wa Kanda ya Ziwa. Nia ya Serikali ni njema kabisa wote tunafahamu ya kukomesha uvuvi haramu, lakini kinachofanyika sasa hivi ni kinyume na ni mambo ambayo hayapo kabisa hata kwenye sheria zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze Mawaziri, kazi kweli nzuri wanafanya na kubwa lakini kuna watu ambao wapo huko site, kuna task force imeundwa. Hii task force kinachoendelea huko mikoani mwetu, naongelea Mkoa wa Mwanza ni hatari kubwa kabisa kabisa. Nia ya Mheshimiwa Rais wetu ni njema ya kuwaokoa na kuwasaidia wanyonge lakini kinachofanyika ni kuendelea kuwakandamiza na kuwaumiza na kufanya uvuvi usiwepo kabisa kwenye mkoa wetu.

Naomba niweze kukupa mifano ambayo inaendelea kwenye Mkoa wetu wa Mwanza. Ni kweli nyavu zimechomwa ambazo zilikuwa zinajulikana nyavu haramu sawa tumekubali. Hata hivyo, mpaka sasa hivi tunavyoongea hizo nyavu halali ambazo zinatakiwa ziwepo hakuna nyavu. Nyavu zimekuwa kama madawa ya kulevya. Sasa hivi nyavu zinauzwa kwa magendo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawa watu ambao wako huko site, hiyo task force ambayo naiongelea, wanashika watu, wanawanyanyasa watu, wanakuwa na maskari wanatoza faini ambazo hazipo kwenye sheria wala kanuni wala taratibu yoyote ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mifano; kuna baadhi ya wavuvi ambao wameshikwa na Mheshimiwa Waziri nimshukuru kwa sababu ni msikivu tumeongea naye na anasaidia baadhi ya mambo. Mtu anakamatwa kwenye gari ya samaki anaambiwa hauna koleo la plastiki. Faini ya koleo hili la plastiki ni shilingi milioni tano; na consistency haipo. Mmoja atashikwa leo ataambiwa faini milioni tano, mwingine atashikwa kesho anaambiwa ni shilingi milioni mbili, mwingine anashikwa kesho kutwa anaambiwa faini milioni kumi, tunakwenda wapi kama Taifa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wote tunajua ugumu wa ajira uliopo. Watu hawa ni watu ambao wengine niseme ni watu wa chini kweli wanaofanya kazi za uvuvi. Watu hawa wameamua kujiajiri lakini ajira imekuwa ya matatizo. Tumeongea sana humu ndani lakini hiyo operation bado inaendelea na inaendelea kwa nguvu na inaumiza wananchi wetu kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri Serikali, kuna haja na umuhimu wa kukaa na kuangalia haya mambo yanayoendelea huko, mambo yanayoendelea ni mabaya ni mabaya, ni mabaya na unyanyasaji wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuongelea suala ya madawa ya kulevya. Niipongeze sana Serikali, imeleta juzi hapa sheria ambayo tumeipitisha ambayo imesaidia kudhibiti na kupunguza madawa ya kulevya kwa kiasi kikubwa sana kwa upande wa Bara. Hata hivyo kwenye hii hotuba ya Kamati ya UKIMWI pia tumeiona kiwango kikubwa sana cha kudhibiti kwa upande wa Bara sasa hivi na kazi kubwa sana inafanyika na watu hawa wa Mamlaka ya Dawa za Kulevya. Hata hivyo kinachoendelea kwa upande wa ndugu zetu upande wa Zanzibar, wafanyabiashara hawa wengi wamehamia upande wa Zanzibar kwa sababu ya sheria kali ambazo zilizowekwa kwa upande wa Bara.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, naiomba sasa Serikali ifike mahali ikae na ndugu zetu wa Zanzibar, waweke sheria ambazo zitakuwa ngumu kwa pande zote mbili ili kama tumeamua kudhibiti na kukabiliana na madawa ya kulevya iwe kwa pande zote mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuongelea kuhusu suala la UKIMWI. Asilimia100 za fedha za maendeleo ya fedha za UKIMWI zinatoka nje, sisi kama nchi hatujatenga fedha yoyote ya masuala ya UKIMWI. Kuna haja sasa kama Serikali ifike mahali tuanze kutenga fedha za ndani ili tuweze kuwasaidia Watanzania hao wengi na hili ni janga la kila mmoja wetu. Nadhani kama hatujaguswa binafsi tutakuwa tumeguswa kwa ndugu zetu na familia zetu kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kuna haja kama Serikali kujipanga na kutenga fedha za ndani ili tuweze kuendelea kudhibiti na kupunguza maambukizi mapya ambayo yanazidi kuongezeka kwa kasi.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali pia kwa kuanzisha huu mfuko wa UKIMWI. Tumeanzisha huu Mfuko na tukatenga fedha bilioni 5.5 kwa mwaka wa fedha 2016/2017, lakini mpaka dakika hii tunayoongea hakuna fedha yoyote ambayo imekwenda. Sasa hawa watu watafanyaje kazi bila kuwa na fedha. Kwa hiyo naona kuna shida na kuna umuhimu sana wa kuliangalia hili ili tuweze kusaidia Watanzania wengi kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, napenda niongelee tena kidogo kuhusu suala la elimu. Research nyingi ambazo zimefanyika, zinaonyesha kuna uhusiano mkubwa sana kati ya sayansi na maendeleo. Leo hii tunavyoongea, si maneno yangu hata ni juzi tu Rais wa Awamu ya Tatu Mheshimiwa Benjamini Wiliam Mkapa amesema elimu yetu inaporomoka; na huu ni ukweli usiopingika. Tunahitaji mjadala mkubwa kama Taifa, tuweze kukaa na kutengeneza mfumo wa elimu.

Mheshimiwa Spika, nia na madhumuni ya nchi yetu ni kutengeneza Tanzania ya viwanda. Hata hivyo, hatuwezi kupata viwanda bila kuwa na wataalam, bila kuwa na Watanzania wenye uelewa mzuri wa kuweza kutimiza azma hii nzuri ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimniwa Spika, hali ya Walimu wetu sasa hivi ni mbaya, motivation ni zero. Wanafanya kazi kwa kwa sababu hawana options nyingine, lakini kiuhalisia wanaenda hawana wanachokifanya kwa sababu maslahi hayapo, maslahi yao bado ni duni, wana madai yao ambayo hayajalipwa kwa muda mrefu. Kwa hiyo ifike mahali sasa kama nchi tutengeneze mfumo mzuri ili kuweza kuwa-motivate hawa watu kwa vile hawa ndio wanaotufundishia watoto wetu.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa nia yake nzuri kabisa ya kuifanya elimu bure, ni kweli elimu bure imepatikana na leo hii tunavyoongea watoto wengi sana wameenda kwenye shule zetu. Hata hivyo wingi wa watoto hao pia umekuwa ni tatizo. Chumba kimoja kinakuwa na watoto zaidi ya mia mbili. Katika hali ya kawaida watoto hawa hawawezi kuelewa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Spika, tuna upungufu mkubwa wa madarasa, tuna upungufu mkubwa wa Walimu wa primary, tuna upungufu mkubwa wa Walimu wa sayansi. Kwa hiyo Waziri wa Elimu atakapokuja kutujibu hapa atueleze kuna mkakati gani wa Serikali wa kuweza kuyabadilisha haya mambo ili tuweze kuwa na elimu bora.

Mheshimiwa Spika, naomba kuzungumzia uwanja wetu wa ndege wa Mkoa wa Mwanza. Wote mnafahamu Mwanza ndilo Jiji la pili kutoka Dar es Salaam, lakini uwanja wetu wa ndege sehemu yetu ya kusubiria abiria kwa kweli inasikitisha, siyo hadhi ya Mkoa wa Mwanza. Naomba tuje tupate mkakati wa Serikali ni lini sasa uwanja huu utarekebishwa na tutatengenezewa kiwanja ambacho kitakuwa na hadhi ya Jiji la pili la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kuna lingine nataka kuzungumzia kuhusu masuala ya nishati ya mkaa. Wote tunafahamu zaidi ya asilimia 90 ya Watanzania wanatumia mkaa majumbani kwao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Wizara yetu ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Nianze kwa pongezi kwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa maamuzi yake makubwa na ya msingi kabisa ya kuamua kutoa elimu bila malipo. Hili jambo limekuwa zuri na limeongeza sana wanafunzi kwanza kuanzia shule ya msingi na sekondari, lakini jambo hili limekuja na changamoto nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto kwenye miundombinu ya elimu msingi, kwenye shule zetu za primary kuna upungufu wa madarasa kwa asilimia 85, kuna upungufu wa vyoo kwa asilimia 83, kuna upungufu wa walimu kwa asilimia 60. Sekondari vivyo hivyo, hii ni kutokana na ripoti ya CAG, madarasa kwenye sekondari ni asilimia 52, maabara asilimia 84, madawati asilimia 86.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwiano wa ongezeko la wanafunzi kuanza shule na uwiano wa miundombinu bado havilingani. Tumeongeza wanafunzi kwa asilimia 17 lakini mpaka hivi tunavyoongea ni asilimia moja tu ya madarasa ndiyo yameongezeka, inafika mahali darasa moja linakuwa na wanafunzi 100 – 150. Kiuhalisia hili suala linakuwa gumu na vilevile hatuwezi kupata elimu ambayo itakuwa bora kwa uwiano mwalimu mmoja na wanafunzi 150. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wenzangu wamezungumzia kuhusu upungufu wa walimu. Kuna upungufu mkubwa sana wa waalimu, hususan walimu wa sayansi. Nikitoa mfano Wilayani Mwanza kwenye Jimbo la Buchosa, kuna shule hakuna kabisa walimu wa sayansi na mwisho wa siku tunakuja tunategemea wanafunzi wa form two wafanye mitihani ya Taifa ya NECTA ambayo inahusisha na masomo ya sayansi. Hawa wanafunzi tunawadahili vipi kama hakuna mwalimu na mwisho wa siku tunataka wafanye mitihani na wafaulu mitihani yao. Hili suala linakuwa ni gumu kwa kweli na nadhani ifike wakati muafaka sasa tuangalie kwa jicho la kipekee suala la kuongeza walimu shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kuzungumzia pia kuhusu suala la elimu kuwa chini ya TAMISEMI. Ni maoni yametolewa na Wabunge wengi na pia Kamati pia imezungumzia hili suala ifike mahali sasa, suala la elimu lijitegemee kama elimu. Itakuwa rahisi ku-monitor na itakuwa rahisi vilevile kufuatilia, ufuatiliaji wake itakuwa tunajua ni nani yuko accountable na hili suala. Mwisho wa siku ndiyo tunaongea shule hazina walimu, ukienda kwa Mheshimiwa Waziri wa Elimu anakwambia siyo la kwangu liko TAMISEMI, lakini ingekuwa chini ya Wizara moja inakuwa rahisi na uwazi pia ungepatikana ukaonekana na kujua ni namna gani tunaangalia suala la elimu kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo limeongelewa ni suala la adhabu ambayo imetolewa mwaka jana baada ya mitihani kuibiwa. Kilichofanyika kwenye shule za private ni kama uonevu. Shule za private baada ya mitihani kuibiwa, mitihani imerudiwa na shule za private zimefungiwa haziwezi kufanya mitihani kwenye shule zao. Wanafunzi inabidi watoke shule moja waende shule nyingine wakati wa kufanyia mitihani, lakini kwenye Wilaya ya Chemba, Halmashauri ya Chemba ni shule pia zimefutiwa mitihani lakini kwa sababu ni shule za Serikali, bado wao wanafanya mitihani kwenye shule zao. Naomba Mheshimiwa Waziri akija kujibu atuambie hii adhabu imetokana na nini na kwa nini kunakuwa kuna double standard. Shule za Serikali zinapewa adhabu tofauti, shule za private zinapewa adhabu tofauti, Mheshimiwa naomba ukija ku-wind up utuambie ni nini kinapelekea suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hiki kitabu cha ripoti ya wizara, page namba 146 naomba nisome, kinaandika, kuandika muhtasari wa lugha ya Kichina kidato cha tano na cha sita ambayo inafundishwa katika shule za sekondari kumi na sita, zimetajwa shule hapo. Naomba ifike mahali tuwe na kipaumbele tujue tunataka nini. Kama mpaka leo…

MWENYEKITI: Malizia, malizia!

MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia. Kama mpaka leo hatuna vitabu vya darasa la kwanza mpaka la tatu kwenye shule za primary, hatuna Mtaala ambao unatuelezea kwenye shule za msingi, sasa inakuwaje tunaanza kuanza kuandika Kichina na tunatengeneza muhtasari wa South Sudan wakati hapa penyewe Tanzania ambapo darasa la kwanza mpaka la tatu hawana vitabu mpaka leo.
Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA ARDHI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nianze kwa kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuweza kuhitimisha hoja ya Kamati yetu ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Kamati yetu imechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wanane. Pia nawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri wote; Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, na Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii kwa kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, nikianza na Mheshimiwa Jitu Soni, amezungumzia suala la miundombinu mibovu katika hifadhi zetu za Taifa. Hili suala ni kweli, nasi kama Kamati ya Maliasili tumelizungumzia kwenye Kamati yetu na tukatoa mapendekezo kwa Serikali ifanye utaratibu wa haraka kushughulikia miundombinu yote ya hifadhi zetu.

Mheshimiwa Spika, wote tunafahamu Wizara ya Maliasili ina mchango mkubwa sana wa pato la Taifa katika nchi yetu. Kwa hiyo, kuboresha miundombinu hii kutawezesha watalii wetu wa nje na ndani kufika kwenye hifadhi zetu kiurahisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Jitu Soni pia alizungumzia miradi ya ujirani mwema ya TANAPA. Mawazo yake ni mazuri na nina imani Wizara imechukua maoni yake na itayafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, mchangiaji wa pili alikuwa Mheshimiwa Mch. Msigwa ambaye alizungumzia masuala ya utalii kuhusu Wizara kutofanya jukumu la kutangaza watalii kutoka nje kwa sehemu kubwa linalofanywa na makampuni ya utalii. Nianze kwa kuonyesha kwanza masikitiko makubwa kwamba Mheshimiwa Msigwa ndio Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii na jitihada zote zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii hazioni.

Mheshimiwa Spika, kazi inayofanywa na Wizara ni kubwa, watalii wameongezeka Mheshimiwa Waziri ametuambia kutoka milioni moja mwaka 2015, mpaka milioni 1.5 mwaka 2020 ambayo tupo. Suala lingine ambalo Mheshimiwa Msigwa alizungumzia ni kuhusu wasanii wetu wa ndani. Napenda nimwambie Mheshimiwa Mch. Msigwa, utalii ni two way traffic; tunahitaji watalii wa nje na vilevile tunahitaji sana watalii wa ndani. Tanzania ina watu zaidi ya milioni 50 na mpaka sasa tunavyozungumza ni watalii 600,000 tu wa ndani ambao ni Watanzania kwa takwimu za mwaka 2018.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili ni jukumu letu sote kama Waheshimiwa Wabunge na Wawakilishi wa wananchi wa Tanzania ambao tumo humu ndani kulisemea na kufanyia kampeni nchi yetu. Wote tuendelee kusema na tuwashawishi Watanzania wenzetu waende kutembelea hifadhi zetu kwa sababu pia tunahitaji sana watalii wa ndani ambao wanatokana na sisi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mch. Msigwa vilevile amezungumzia masuala ya wasanii wetu wa ndani na akatoea mfano wa Steve Nyerere. Mheshimiwa Waziri amelizungumzia hili vizuri, lakini kwa kuongezea tu, huyu Steve Nyerere ana segment ya watu ambao wanamfuata na ni muhimu pia kwa hao watu. Kwa hiyo, ni vizuri tusiwabeze wasanii wetu wa ndani kwa sababu wanakubalika ndani na vilevile na nje ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Getere amezungumzia kuhusu utalii wa ndani, nadhani nimeshalizungumzia hilo. Pia ameongelea suala la TANAPA ambalo tumeshalileta kwenye Bunge lake Tukufu. Ni katika miaka minne yote ambayo nimekuwa kwenye hiyo Kamati, tumelizungumzia mara kadhaa, tumeomba TANAPA wapunguziwe tozo kwa sababu hifadhi zimeongezeka kutoka hifadhi 15 zilizokuwepo mpaka 22 sasa hivi tunavyozungumza na hifadhi tano tu ndizo ambazo zinaweza kujiendesha na hifadhi mbili ya Serengeti na Kilimanjaro ndizo ambazo zinachangia kuendesha hifadhi nyingine ambazo haziwezi kujiendesha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mzigo walionao ni mkubwa. Ni vyema kabisa Bunge lako Tukufu tukaishauri Serikali kutafuta namna bora ambayo itaiwezesha TANAPA kuweza kukidhi mahitaji waliyonayo. Kwa mfano, mdogo tu ambao tunaweza kuutoa, watu hawa wa TANAPA wanafanya SCR (Social and Cooperate Responsibilities) lakini katika kazi ambazo wanazifanya za kijamii kwa mfano wakijenga shule au wakifanya shughuli yoyote ya kijamii bado wanatozwa kodi kwenye kazi ambazo wamezifanya; na kazi hiyo wanazozifanya ni kubwa na ni nyingi. Kwa hiyo, kwa kuwapunguzia tu hata hiyo, tutakuwa tumepunguza mzigo ambao utawawezesha kwenda kufanya mambo mengine na kwenye hifadhi nyingine kuziboresha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchangiaji mwingine anayefuata ni Dkt. Kiruswa, amepongeza Wizara na Serikali kwa kazi inayofanya. Mheshimiwa Kiruswa pia amezungumzia suala upimaji wa ardhi ambayo napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwa mara ya kwanza, kazi ya kupima na kupanga ardhi ya nchi hii imepewa mamlaka hiyo. Siku zote traditionally imekuwa kazi ya TAMISEMI, lakini ukweli ni kwamba mpaka leo ardhi ambayo imepimwa ya nchi hii ni chini ya asilimia 20 ambayo kwa kweli siyo kitu kizuri. Ndiyo maana tumekuwa na migogoro mingi ya ardhi, wafugaji na wakulima. Kwa sababu ardhi kubwa ya nchi hii haijapimwa na kupangwa.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuona umuhimu wa kutenga fedha nyingi sana na kuwapa Wizara ya Ardhi ambayo kuna miradi mikubwa miwili ambayo itakwenda kupima, kupanga maeneo yote ya Tanzania. Ardhi yote ya Tanzania itapimwa na kupangwa. Hili siyo tu kwamba litaongeza mapato kwa sababu ya kulipia hati ambazo wananchi watakuwa wamepata, lakini vilevile itapunguza migogoro mingi sana ya ardhi ambayo inaendelea katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, maendeleo hayana chama, wote tunafahamu. Naomba kuchukua fursa hii kukuomba kushauri Wabunge wote tuliomo humu ndani ya Bunge hili Tukufu, tuchukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa kumpigia makofi mengi sana san asana kwa kazi kubwa ambayo ameifanya ya kupima na kupanga maeneo yote ya ardhi nchini mwetu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mchangiaji mwingine alikuwa Mheshimiwa Rhoda ambaye amezungumzia suala la vijiji 920 ambalo Mheshimiwa Waziri amelitolea maelezo vizuri kabisa, nadhani amelielewa, nasi kama Kamati tunaunga mkono, lakini ripoti hiyo haijaja rasmi kwenye Kamati yetu na itakapokuja tutaiwasilisha Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Maftaha amezungumzia suala la TAWA. Sisi kama Kamati kweli tunamuunga mkono na tumeliongelea kwenye ripoti yetu, TAWA tangu imeanzishwa bado haijapa sheria na haijajitegemea. Kwa hiyo, kuna mambo mengi ambayo inashindwa kufanya kama mamlaka kwa sababu hawana maamuzi ya kuweza kufanya kama mamlaka kamili. Kwa hiyo, tunaisihi Serikali, tunaiomba Wizara ifanye huu mchakato kwa haraka ili TAWA iweze kupata sheria yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dau amezungumzia suala la viboko wa Mafia; watu wamefariki, hili suala siyo kwa Mheshimiwa Dau peke yake, limejitokeza kwa Waheshimiwa Wabunge wengi, Mheshimiwa Gekul ameshalizungumzia hilo suala Bungeni hapa, Mheshimiwa Mulugo ameshatuambia wazazi wake wote wawili walifariki kwa sababu ya viboko huko Ziwa Tanganyika. Kwa hiyo, hili suala ni muhimu, nami na Kamati yetu tunaomba sana hili suala la viboko lifanyiwe utaratibu wa haraka ili tuweze kutatua changamoto hii ambayo inaleteleza vifo kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, sasa naomba Bunge lako Tukufu lipitishe maazimio tuliyoleta mbele ya Bunge lako.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, naafiki.