Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Pauline Philipo Gekul (74 total)

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza.

Pia naomba nitumie nafasi hii kuiomba Wizara ya Mifugo kabla sijauliza maswali yangu waje wakutane na wadau wa mifugo na wafanyabiashara katika Wilaya yangu ya Longido waweze kutathmini matokeo chanya na matokeo hasi ya operesheni hii ambayo imeingizia Serikali fedha nyingi tu ambazo swali langu la kwanza ninaomba kufahamu kwamba kati ya fedha hizi ambazo zimepatikana ni miradi gani ya maendeleo katika sekta ya mifugo ambayo ama imetekelezwa au imepangwa kutekelezwa ili wafugaji hawa waone tija ya fedha hizi zinapoingia Serikalini?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, ninapenda kufahamu pamoja na changamoto ya hawa wanaosimamia operesheni ambao wamedhulumu watu ambao wamekamatiwa mifugo bila kuwa na hatia na wengine wenye hatia waliofilisika, lakini na wao kwa taarifa yangu hawajalipwa stahiki zao. Ni lini Serikali itakwenda kuwalipa stahiki zao kwa kazi kubwa waliyofanya?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa
Spika, Mheshimiwa Mbunge kwanza amehitaji kufahamu ni miradi kiasi gani ambayo imetekelezwa kupitia fedha hizi ambazo tunazikusanya.

Mheshimiwa Spika, sisi Wizara yetu katika Vote ya 99 ambayo tunapangiwa Bunge hili tukufu bajeti yetu ya maendeleo ni shilingi bilioni 5.6 lakini katika hizo bajeti shilingi bilioni 5.6 tunakarabati minada, tunarekebisho majosho, mfano kwenye bajeti kiasi cha majosho 75 kwa Halmashauri nchini zinakarabatiwa, lakini majosho 20 yanajengwa kwa shilingi milioni 500, lakini pia tunajenga kiwanda cha chanjo pale Kibaha TVLA zaidi ya shilingi milioni 600.

Mheshimiwa Spika, fedha tunapopangiwa na Serikali kila Wizara na sisi tunapopokea na kwa mwaka huu wa fedha shilingi bilioni tano zinaendelea kurudi kwa wafugaji wetu kwa kukarabati miundombinu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amependa kufahamu swali lake la pili kwamba watumishi hao wanaofanya operesheni wanakuwa wanafanya kwa awamu mbalimbali, lakini wanahitaji malipo. Serikali imekuwa ikiwalipa watumishi hao ambao wamekuwa wakifanya operesheni ya kudhibiti utoroshwaji wa mifugo na madeni yao yameshapunguzwa, sasa watumishi hao kote nchini wanadai shilingi milioni 662.9 na hizo fedha zimeshakaguliwa Mheshimiwa Mbunge, hivi karibuni mchambuzi ukishakamilika Wizara ya Fedha watalipa fedha hizo.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa
Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa Serikali ina mpango wa kununua meli nane kubwa za uvuvi, ambapo nne zitaenda Zanzibar na nne zitakuwa Tanzania Bara. Je, ni lini meli hizo zitanunuliwa ili zianze kutoa ajira na kutoa huduma kwa wananchi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa katika jibu lake la kwanza ameelezea hiyo ujenzi wa bandari ya uvuvi, ningependa kujua je, upande wa pili wa Muungano utashirikishwa vipi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa
Spika, ununuzi wa meli nane ambazo zimesemwa katika ahadi yetu ya Serikali ununuzi huu utaanza hivi karibuni kwa kuwa Serikali sasa iko katika mazungumzo na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo, maelezo na mazungumzo hayo yanaendelea, yakishafanyika Wizara ya Fedha sasa itaingia makubaliano na mfuko huu ili ununuzi uweze kuanza.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge alihitaji kufahamu kazi hii ya ujenzi wa bandari ambayo inaendelea kwa upande wa Bara na upande wa Zanzibar nini kinaendelea.

Mheshimiwa Spika, naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba mazungumzo haya yanapoendelea kwa upande wa Bara pia upande wa Zanzibar wameanza mazungumzo na nchi ya Comoro na bandari ya Zanzibar pia itaanza kujengwa na ikijengwa maana yake ajira hizi sasa zitatolewa kwa pande zote.
MWANTATU MBARAK KHAMIS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kabla ya kuuliza swali la nyongeza kwanza nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali kwa jitihada za kuona umuhimu wa kusaidia kuimarisha shughuli za michezo kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka 2021/2022, Bunge liliidhinisha shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya shughuli za michezo. Je, kwa bajeti hii, kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya kuendeleza shughuli za michezo kwa watu wenye ulemavu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliiagiza Wizara kuimarisha michezo kwa wanawake na nimeona katika vyombo vya habari kwamba Wizara inajiandaa kutayarisha tamasha ambalo litajumuisha wanamichezo wanawake wa Tanzania nzima. Niipongeze sana Wizara kwa kufanikisha hilo. Swali langu, kwa vile michezo hii inajumusiha wanawake wa Tanzania nzima, je, maandalizi yamezingatia vipi ushiriki wa wanawake wakiwemo wanawake wenye ulemavu kutoka Zanzibar? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantatu Mbarak Khamis, Mbunge kutoka Baraza la Wawakilishi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza amehitaji kufahamu katika Mfuko wetu wa Maendeleo ya Michezo ambao Bunge hili Tukufu mmetupitishia zaidi ya 1.5 billion, je, fedha hizi zitakwenda kuwa-support watu wenye ulemavu? Naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba watu wenye ulemavu katika Wizara yetu ni watu wa kipaumbele. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi kabisa kwamba pale ambapo watakuwa wanahitaji support ya Wizara, hasa kwa michezo ya Kimataifa ndiyo sababu ya fedha hizi kupitishwa na sisi tutaendelea kuwapa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, pia siyo fedha hizi tu tuna fedha kwa ajili ya Mfuko huu kupitia michezo ya bahati nasibu, maana yake mfuko huu utaendelea kutunishwa. Kabla ya hapo fedha zilikuwa chache, tulikuwa na takribani zaidi ya milioni 200 kwenye Mfuko kwa ajili ya kuwa-support, lakini kwa sasa kwa fedha hizi maana yake wao watakapofuzu kupitia kwenye vyama vyao sisi tutaendelea kuwapa kipaumbele watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, alihitaji kufahamu kwenye tamasha hili la michezo kwa wanawake ambayo Wizara yetu jana pia tumezindua Kamati ya kusimamia tamasha hili ambalo litasimamia michezo kwa wanawake, je, watu wenye ulemavu wamepewa nafasi kiasi gani.

Naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba watu wenye ulemavu katika tamasha hili watashiriki kupitia michezo yao ambayo wanacheza. Kwa sasa kuna timu ya mpira wa kikapu na wanariadha watashiriki katika tamasha hili na pia tumeshirikisha wote.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe rai kwa Watanzania wote hili tamasha litakapoanza mwezi huu wa Septemba kuanzia tarehe 16 na kuendelea, tushiriki kwa pamoja ili tuweze kumuenzi Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwenye suala zima la kunyanyua wanawake katika michezo. Nitoe rai kwa Wabunge wenzangu, tutaleta mwaliko kwako Spika, naomba tushiriki. Najua tunacheza netball, lakini kamba na michezo mingine wanawake tujitokeze na tamasha hili litakuwa endelevu.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nitumie nafasi hii kushukuru majibu mazuri sana ya Serikali. Swali langu la nyongeza;

Je, Serikali ina mpango gani wa kutambua kundi la Video Vixens kama makundi mengine ya sanaa kupitia Sheria Na. 7 ya Mwaka 1999; kwa sababu Mheshimiwa Waziri amekiri kwamba tayari kundi hili halitambuliki rasmi bali kundi linalotambulika ni kundi la wanamuziki; na kwamba mikataba ya watu hawa haitambuliki, kwamba inayotambulika ni ya kundi la wanamuziki pamoja na makundi mengine, na siyo kundi la Video Vixens? Je, kupitia Sheria hiyo Na. 7 ya Mwaka 1999 tunawasaidiaje vijana hawa kuweza kutambulika?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa kundi la Video Vixens ambalo linachukua Video Kings pamoja na Queens, na kwamba ni kundi linalochukua vijana wengi zaidi; sasa Serikali haioni haja ya kuwasaidia kuwatengenezea mikataba mizuri ili vijana hawa wasipitie changamoto wanazozipitia; kwa sasa hivi kwa sababu wanafanya kazi kubwa lakini wanalipwa ujira mdogo na wananyanyasika?

Nikisema wananyanyasika nadhani Waheshimiwa Wabunge tunaelewana. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Asia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye majibu yangu ya awali na ya msingi nilieleza kwamba kwenye Sheria yetu ya Mwaka 1999 vijana hawa walikuwa hawajatambuliwa, lakini kwa sababu ya umuhimu wa kazi yao; ilibidi sheria hii tuirekebishe mwaka 2019, Kifungu na. 47(b) ndicho kikatambua sasa ikaingiza mkataba, kwamba ni lazima hawa vijana ambao wana-perform na wale owners wa kazi ile waweze kutambuliwa, na mikataba yao COSOTA iiangalie.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilihakikishie Bunge lako Tukufu na wasanii kwamba hawa vijana hawajaachwa, sheria inawatambua. Na hata pale ambapo vijana hawa wanadhulumiwa COSOTA inaingilia kati kwa sababu ile mikataba inakuwa imeshapitia kwao. Mimi niwahakikishie kwamba wakati tunafanya marejeo ya kanuni maoni yamechukuliwa kote na hatujapata malalamiko so far kwamba wanaonewa.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kuendelea kuwalinda kwa sababu – swali lake la pili – tunapitia Kanuni yetu ya mwaka 2003 kuona jinsi gani tuboreshe mpaka hata mgawanyo tunaotoa wa fedha kwa wamiliki au wasanii wetu; maana kama kuna jambo lolote within marekebisho yale Mheshimiwa Mbunge, yatakwenda kuangaliwa wakati Kanuni hiyo haijafika mwisho, maana wana nafasi ya kutoa tena maoni yao.
MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini kwenye TFF ukomo wa uongozi ni vipindi vitatu vya miaka minne minne. Lakini, kwenye TOC hakuna ukomo. Je. haoni inazuia uhuru wa watu wengine kugombea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwa upande wa TFF wao wamekwenda vizuri kama alivyosema lakini TOC wanaendelea kufanya marekebisho katika katiba yao. Katiba yao Mwaka 2019 walirekebisha, 2020 msajili aliweza kuipitisha Novemba na katika marekebisho ambayo amefanya sasa, wameweka kipengele cha kwamba, mtu akigombea nafasi ya Urais basi ahudumu kwa term 3 akishahudumu kwa term 3 ya miaka minne minne ya miaka 12, baada ya hapo asirudie kugombea nafasi hiyo bali sasa apande juu aende IOC au kwenye nafasi zingine. Kwa hiyo, wameendelea kuboresha vile vipengele ambavyo vinaminya uhuru wa watu wengine na wengine kuendelea kugombea. Ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kama ilivyo kwa Chama cha TFF kwenye eneo la ngumi kumekuwa na ubabaishaji mwingi sana kwa kitu kinachoitwa Rais wa ngumi.

Je, Serikali ina mpango gani wa kusimamia uongozi huu unaokaa kwa muda mrefu bila kufuata katiba kama inavyosema? Ahsante kwa kunipa hiyo nafasi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara kupitia BMT lakini kupitia kwa Msajili, tunaendelea kufuatilia hizi katiba ambazo wamechomeka vipengele ambavyo vinawafanya watu kuendelea kukaa madarakani. Mheshimiwa Mwakagenda suala lako tunalipokea na pia nitafanya ziara katika maeneo hayo na tutapitia katiba yao pia kwa upya tuone ni wapi wameweka vipengele hivyo. Nikuhakikishie kupitia msajili tutaangalia na tutashauri lakini pia wanachama, mtushauri pale ambako mnaona hizi katiba zinakandamiza uhuru wenu katika vyombo hivyo ambavyo mnashiriki vya kimichezo. Tuko tayari kupokea ushauri wenu.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa nchi nyingi sana kama alivyoeleza zimeamua kwa dhati kuwa na mtaala wa Kiswahili na ukizingatia pia tunao vijana wengi wabobezi kwenye eneo hili la Kiswahili. Serikali inaweka mkakati gani kuhakikisha vijana hawa wanapata ajira kwenye maeneo hayo ili tusije kuzidiwa na nchi zingine za Jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Kumekuwa na ongezeko kubwa sana la misamiati ambayo inatokana na matukio mbalimbali na misamiati hii inaweza kuathiri lugha yetu ya Kiswahili. Serikali ina mkakati gani wa kukabiliana na ongezeko la misamiati hii? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza Mheshimiwa Mbunge amehitaji kufahamu Serikali inajipanga vipi kuwasaidia vijana wetu wapate ajira kupitia lugha hii ya Kiswahili.

Mheshimiwa Spika, katika majibu yangu ya awali nilieleza kwamba Serikali ilishaanza mazungumza na Balozi zetu kupitia Wizara ya Mambo ya Nje kuhakikisha kwamba hawa wataalam ambao wamezamishwa, wameeleweshwa lugha ya Kiswahili na namna gani wafundishe wageni waweze kushirikiana katika Balozi zetu na madawati hayo yaanzishwe.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kupitia BAKITA tunalifahamu jambo hili na nimesema kwamba tuna wataalam zaidi ya 1318 ambao wapo tayari na tumekuwa tukiwasaidia na wamekuwa wakiwasiliana na BAKITA kwa karibu waweze kupata ajira hizo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili Mheshimiwa Mbunge alitaka kufahamu ni kwa kiasi gani Serikali inaangalia misamiati inapokuwa imezalishwa ni kwa kiasi gani tunafuatilia kama kuna mabadiliko ya mazingira. Mheshimiwa Mbunge nikuhakikishie kwamba Serikali kupitia BAKITA tumekuwa makini sana. Panapotokea mabadiliko yoyote ya kimazingira, ya kieneo au mazingira ya matukio yoyote BAKITA wamekuwa wakitafuta misamiati mbalimbali na kuhakikisha kwamba tunasanifisha misamiati hiyo lakini pia tunachapisha.

Mheshimiwa Spika, mfano, hivi karibuni nchi yetu imekumbwa na ugonjwa wa Covid lakini BAKITA tumejidhatiti na tumeshasanifisha covid – 19 inaitwaje kwa Kiswahili ambayo inaitwa UVIKO – 19. Nitoe rai kwa Watanzania kwasababu tunapenda lugha yetu tuhakikishe tunatumia lugha hii ya Kiswahili badala ya kusema covid – 19 tunaweza tukasema UVIKO – 19. Naomba kuwasilisha.
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa uvumbuzi wa vipaji, lakini pia na uendelezaji wa vipaji unapaswa kuanzia ngazi ya chini kabla ya kufika kwenye National level hasa kwenye shule zetu za sekondari, vyuo na huko halmashauri kwa ujumla. Je, Serikali haioni haja kwamba inapaswa kutenga fedha za kutosha kwenye bajeti yake ili kuendeleza vipaji vya michezo mashuleni, vyuoni na huko chini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; tumesikia kwamba, Serikali imeanzisha combination za elimu ya michezo (physical education). Nataka kujua utekelezaji wa jambo hili umefikia wapi mpaka sasa? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vuma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge maana yeye ni mdau mkubwa wa michezo, lakini pia niwapongeze Wabunge wote pamoja na Waheshimiwa Madiwani katika halmashauri zao kwa jinsi ambavyo wamekuwa wakishirikiana na Wizara hii kwa suala zima la michezo. Swali lake la kwanza alitaka kufahamu ni kwa kiasi gani Serikali inatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha michezo katika ngazi za chini inapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo ni la muhimu sana. Sisi kama Wizara nimesema tangu mwaka 2019/2020 tumeanza, lakini nitoe rai sasa kwa Waheshimiwa Madiwani na Waheshimiwa Wabunge katika ngazi za halmashauri, fedha za michezo zitengwe. Kwa hali ilivyo sasa ni Madiwani na baadhi ya wadau wanahangaika na hili suala, lakini halmashauri zetu zitenge fungu chini ya Idara ya Elimu Msingi kwa ajili ya kuhakikisha michezo inadumishwa katika maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili alitaka kufahamu mkakati tulionao wa Wizara kuanzisha hizi combinations za michezo kwa A Level zimefikia hatua gani. naomba nimjulishe Mheshimiwa Vuma kwamba, Kamati ilishaundwa kati ya Wizara ya Elimu, Wizara ya Michezo pamoja na TAMISEMI na ipo site ikitembelea zile shule 56 za msingi na sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Kamati hiyo kuleta majibu maana yake tunaendelea na zile shule ambazo tumeshazitambua ikiwemo Shule za Kibiti, Mpwapwa na Makambako ili kuanzisha sasa hii combination na tupate network kuanzia msingi mpaka vyuo vikuu. Endapo kazi hii itakuwa imekamilika itasaidia sana kutoa mafunzo kwa vijana wetu kuhusu masuala ya michezo. Ahsante. (Makofi)
MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

La kwanza, kwa kuwa ujenzi huu maazimio ya kikao hiki yaliuweka kusimamiwa na Serikali ya Tanzania na kwa kuwa ujenzi wa sanamu hii ya Baba yetu wa Taifa yatasaidia kutangaza utamaduni wa Tanzania na mchango mkubwa wa Baba yetu Taifa katika kupigania uhuru wa nchi mbalimbali za Afrika. Ningependa Serikali ituambie ni kwa nini tangu mwaka 2015 yalipopitishwa maazimio haya mpaka sasa ujenzi huu haujaanza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, kwa kuwa maamuzi haya au maazimio haya ya kikao yalitoa kipaumbele kwa wakandarasi wazawa wa Tanzania kuwa wa kwanza kabisa kupewa tender hizi na kwa kuwa mwaka 2018 tender hizi zilipotangazwa ilionekana hakuna wasanii/ vijana Watanzania wenye vigezo vya kutosha kimataifa kujenga sanamu hii. Basi Serikali ningependa ituambie ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inakuza ujuzi na uwezo wa wasanii wa Tanzania ili pale tender kama hizi zinapojitokeza kimataifa.

MWENYEKITI: Swali.

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo swali hili.

Ningependa Serikali itueleze ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wasanii wa Tanzania pale ambapo tender hizi za kimataifa zinatangazwa tena wanajengewa uwezo ili nao wapate kushiriki kama Nchi zingine? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kamani kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kamani kwanza amependa kufahamu kwa nini delays. Nipende kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba mchakato huu wa kujenga sanamu ya Baba wa Taifa Ethopia Addis, ilikuwa ni wazo zuri sana kwa wakuu wa nchi za SADC kuipa heshima Taifa letu lakini kumpa heshima Baba wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, delays hizi zinatokana na mchakato; kwanza Kamati lazima ziundwe za kitaifa lakini pia kupitia Kamati hizo lazima zikae na familia ya Baba wa Taifa ili kupata prototypes zile ambazo zinahitajika tatu kabla ya ujenzi wa sanamu hii. Lakini pia conditions ambazo SADC imetupa ni kwamba lazima picha ya Baba wa Taifa iwe ni enzi hizo miaka hiyo wakati anapigania uhuru wa Taifa hili.

Kwa hiyo michakato hii, pamoja na conditions mpaka sasa inaendelea vizuri lengo ikiwa ni kuhakikisha sanamu tutakayoijenga pale Ethiopia iwe ni samanu ambayo inaakisi picha halisi ya Baba wa Taifa. Kwa hiyo, michakato hii inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lako la pili la Mheshimiwa Ng’wasi, ni kwa kiasi gani wasanii wetu tunawashirikisha na tunawajengea uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeza Mheshimiwa Mbunge pamoja na Wabunge kwamba mlitupitishia bajeti katika Bunge hili ya zaidi ya shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya sanaa na utamaduni. Kupitia mfuko huu Mheshimiwa Mbunge tukuhakikishie tutaendelea kuwajengea uwezo wasanii wetu, lakini kwa kuwa Tanzania tumepewa nafasi ya kusimamia ujenzi huu wa sanamu ya Baba Taifa, meneja wetu huyu aliyeteuliwa pia amepewa nafasi mbili ya kwenda na wasanii wetu Ethiopia waweze kuona kwamba wasanii wetu waweze kujua teknolojia hii. Kwa hiyo, hii ni Wizara yetu tunalifanyia kazi kwa karibu kupitia Mfuko wa Utamaduni na Sanaa.


MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; kwa kweli majibu haya sioni kama yatatusaidia kuinua michezo nchini, naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza, Jimbo la Hai tayari pale Half London tayari tumetenga eneo kwa ajili ya kujenga kiwanja cha michezo.

Je, Serikali ipo tayari sasa kufanya mabadiliko kwenye Sera ya Michezo ili jukumu la kujenga uwanja liwe ni la Serikali Kuu na siyo Halmashauri? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili; Jimbo la Hai tuna vikundi vya sanaa vingi, tuna wasanii wazuri wengi na tayari tumeshaunda jukwaa la wasanii Jimbo la Hai na walezi wetu Mheshimiwa Taletale na Mheshimiwa MwanaFA.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri upo tayari kuambatana na mimi kwenda Hai kukaa na jukwaa la wasanii wa Hai ili kusikiliza changamoto walizonazo?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mafuwe, Mbunge wa Hai.

Mheshimiwa Spika, kwanza Mheshimiwa Saasisha amehitaji kubadilishwa kwa sera hii ili jukumu la kujenga viwanja liwe ni jukumu la Serikali Kuu na si vinginevyo kama ambavyo sera imesema.

Mheshimiwa Spika, Niliarifu Bunge lako tukufu kwamba sera hii imeshawahi kupelekwa kwenye Kamati yetu ya Huduma za Jamii ikidhaniwa kwamba Sera hii imepitwa na wakati na mara nyingi tumekuwa tukiangalia miaka ya sera imetungwa lini lakini siyo validity ya sera hiyo.

Mheshimiwa Spika, sera hii imepitiwa na imeonekana kwamba inashirikisha wadau wote. Serikali Kuu ina jukumu lake, Serikali za Mitaa ina jukumu lake, wadau wana majukumu yao; kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge naomba tushirikiane. Kwa upande wa Serikali Kuu tuna-deal na viwanja vikubwa ambavyo timu zetu za Kitaifa na kimataisa wanaweza wakafika. Lakini Halmashauri zetu zikitenga fedha, Mheshimiwa Mbunge tukishirikiana katika Halmashauri zetu kwa own source zetu, nina hakika kwamba viwanja vitajengwa na wananchi wetu watashiriki katika michezo. Lakini sisi hatukatai kushirikiana na Serikali za Mitaa na nishukuru Bunge mlitupatia shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Michezo, kama bajeti itaendelea kuongezeka sisi tutaendelea ku-support pia huko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameomba tuambatane kwenda Hai kwa ajili ya jukwaa la wasanii, ninakuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaambatana kwa sababu ndiyo maelekezo tuliyopewa tuwahudumie wasanii na mimi nipo tayari tutakwenda tarehe ambazo utakuwa tayari tutafika tutawasikiliza wasanii. Ahsante. (Makofi)
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru; kwa kuwa mmoja wa Wabunge mwenzetu aliwahi kuuliza humu Bungeni kuhusu ukarabati wa viwanja vya michezo na Serikali ikachukua jukumu la kukarabati.

Je, ni lini Serikali itafanyia kazi ombi la ukarabati wa Uwanja Mkuu wa Tanganyika - Ifakara ambao unatumika na Wilaya tatu?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na naomba nijibu swali la Mheshimiwa Abubakari kuwa sisi kama Wizara hatuna tatizo kabisa kushirikiana na Serikali za Mitaa, atakapotuletea maombi haya kwenye Mfuko wa Maendeleo ya Michezo pale tutakapoweza pia tunaweza tuka-support. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaendelea kutoa rai kwa Halmashauri zetu kwamba hili jambo ni serious, tumekuwa tukitenga asilimia 10 ya mikopo, ujenzi wa hospitali, shule zetu, lakini suala la michezo imekuwa siyo kipaumbele. Ninawaomba Waheshimiwa Wabunge tushirikiane na ninawapongeza kwa dhati Wabunge ni wadau wakubwa sana wa michezo. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge Mheshimiwa Rais na Bunge tulipitisha kuondoa kodi kwenye nyasi bandia na hii ilikuwa ni kulenga kuboresha viwanja vya michezo kama sera inavyosema, lakini hali ya miundombinu ya viwanja nchini ni mbaya. Hatuoni mpango wowote wa maksudi wa Serikali kuongea ama na taasisi binafsi ambao wanamiliki viwanja au Halmashauri kuhakikisha tunatumia fursa hii ambayo Mheshimiwa Rais ametupa ya kuweka nyasi bandia nchini.

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa makusudi wa kuboresha hali ya viwanja nchini ili Simba na Yanga ziache kulalamika kutokana na viwanja kama uwanja wa Manungu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, sisi tunalishukuru Bunge kwa kutupitishia exemption kwenye nyasi bandia ya VAT na Baraza letu la Michezo la Taifa (BMT) linaratibu zoezi la Halmashauri zetu wanapohitaji hizo nyasi bandia za grade gani wanaweza wakapata, tunaweza tukaratibu, tutakuunganisha, utapata hizo nyasi Mheshimiwa Mbunge kwa sababu viwango tunavyo vya class A, B, C na bei zake. Kwa hiyo, tushirikiane ili pale mnapohitaji muweze kuzipata.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa kuboresha viwanja vyetu sasa hivi TFF imeingia mkataba pia na Chama cha Mapinduzi ambacho kina viwanja vikubwa katika mikoa yetu. Viwanja kumi tunaenda kuviboresha kupitia mkataba huu ambao tutakuwa tumemaliza kukubaliana nao. Ahsante. (Makofi)
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; mwaka 2017 Kampuni ya SportPesa ilikarabati uwanja wa Benjamin Mkapa kwa thamani ya shilingi bilioni moja na nusu na mwaka 2019 machinery zote tulizotumia kwa ajili ya ukarabati wa uwanja ule ikiwemo seeding tractors, tractors pamoja na special grass cutting machines.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kutumia machine zile kupeleka katika viwanja vyenye uhitaji ili waweze kutumia machine zile? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, Wizara hatuna kizuizi chochote pale ambapo tunapata ombi la kuboresha viwanja vya michezo. Mheshimiwa Mbunge utakapotuletea pia tuta-consider ombi lako. Ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiofichika kwamba ujenzi wa uwanja wa kisasa wa michezo na shughuli za Serikali kwa Makao Makuu ya Dodoma haukwepeki. (Makofi)

Je, Serikali pamoja na majibu ya kusema kutafuta wabia, wadau mbalimbali wa michezo, kwa nini Serikali isiwe na commitment kwamba mwakani katika bajeti tunatenga fedha ili ujenzi huo uanze, ukitilia maanani uwanja hauwezi kujengwa kwa mwaka mmoja?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Innocent kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwisha kujipanga na ndio maana tumeshafanya upembuzi yakinifu kujua kwamba huu uwanja tunaujenga wapi, lakini kwa gharama gani. Huu uwanja unahitaji zaidi ya shilingi bilioni 420 na Serikali tuko kwenye hizo hatua pamoja na maongezi yanayoendelea lakini ndani ya Serikali tunaendelea kutafuta fedha.

Mheshimiwa Spika, nihakikishie Bunge hili tukufu huu uwanja pia ni ahadi ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 na lazima tutaujenga.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwanza kabisa nataka nimpongeze Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa uzinduzi wa uwanja mzuri kule Ruangwa. Sambamba na pongezi hizo nataka niipongeze vilevile timu ya Namungo ambayo ilicheza na ikashinda vizuri sana kwenye ule uwanja wa nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu; je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza juhudi za wananchi katika kuhakikisha kwamba uwanja ule unakamilika?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, na sisi Serikali pia tumeendelea kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuonesha mfano katika suala zima la michezo na kuendeleza miundombinu ya michezo, lakini pia wenzetu wa Ruangwa pamoja na halmashauri yao.

Mheshimiwa Spika, sisi Serikali tumeendelea kuunga mkono jitihada za wadau mbalimbali kuhakikisha pia accessories za michezo kama nyasi bandia, lakini pia vifaa vya michezo kodi inapunguzwa. Sisi tutaendelea kushirikiana na halmashauri na watu binafsi kuhakikisha kwamba tunatengeneza mazingira rahisi ya uwekezaji katika michezo.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwenye Bunge la Bajeti lililopita tulipitisha bajeti ya shilingi bilioni 10 kuweka nyasi bandia kwenye viwanja vya michezo nchini; je, Serikali imefikia hatua gani kwenye kuweka nyasi bandia kwenye viwanja vyetu kwa sababu ligi inaendelea na bado viwanja haviridhishi?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi kuweza kujibu swali la Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika bajeti iliyopita ya Bunge tulipitisha zaidi ya shilingi bilioni 10 kuhakikisha kwamba tunaboresha viwanja vya Arusha, Mwanza, Tanga, Dodoma, Mbeya na viwanja vyetu vikuu vya Mkapa ambavyo sasa vinatumika na vya Uhuru.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara tumeshaanza mchakato kuhakikisha kwamba mwaka huu wa fedha haupiti bila hizi fedha kutumika. Kwa hiyo, Wizara kupitia kitengo chetu cha manunuzi wameshaanza mchakato na tumeendelea kusisitiza kwamba jambo hili la kuboresha viwanja hivi iweze kuanza mapema ili hivi viwanja viweze kutumika. Ahsante.

WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba nilithibitishie Bunge lako tukufu na Watanzania kwa ujumla kwamba viwanja hivi ambavyo Mheshimiwa Sanga amevizungumza havitawekwa tu nyasi bandia na nyasi za kawaida, tutakwenda kuweka viti vya kisasa kabisa. Pia viwanja hivi tunakwenda kuvitengeneza kwa namna ambavyo tunaweza kuvitumia kimataifa na mchakato huu wa ujenzi utaanza mwaka huu. (Makofi)
MHE. SULEIMAN HAROUB SULEIMAN: Mheshimiwa Spika, ahsante sana pamoja na majawabu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina swali moja lenye kifungu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, timu ya Taifa Stars ni timu ya Tanzania na Tanzania ina ligi kuu mbili kwa maana ya kwamba Ligi Kuu ya Zanzibar na Ligi Kuu ya Tanzania Bara. Sasa je, kwenye kuchagua wachezaji kwenye kutafuta wachezaji kuunda timu ya Taifa hauoni haja au hauoni sababu kwamba sasa kocha wa timu ya Taifa kuweza kudhuru ligi zote mbili ili kupata wachezaji wazuri?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; zamani kulikuwa kuna ligi kuu ya Muungano kwa maana ya Super Cup ligi ile iliweza kutoa timu bora na timu nyingi ambazo zilishiriki ligi ile ilitoa wachezaji wa timu ya Taifa Stars. Sasa je, Serikali ina mkakati gani kuweza kurudisha kombe hili? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kunipa nafasi nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Suleiman kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Suleiman amependa kufahamu kwamba katika kuandaa timu za Taifa; je, si vyema timu hizi zikaandaliwa kwa kufatilia ligi zote mbili za TFF pamoja na ZFF.

Mheshimiwa Spika, hili ni dhahiri kwamba tunapochagua wachezaji wa timu ya Taifa kocha hakatazwi kwenda popote kwenye hizi ligi ndani ya Taifa letu na hili limekuwa likifanyika ndio maana wachezaji katika timu yetu ya Taifa wanatoka pia kwa upande wa Zanzibar pamoja na upande wa Bara. (Makofi)

Kwa hiyo hili tutaendelea kuimarisha tukishirikiana na ZFF pamoja na TFF ili kuhakikisha kwamba tunapata wachezaji wazuri na hata katika benchi la ufundi tumekuwa tukiwahusisha wenzetu wa Zanzibar kuhakikisha pia wanatoa mchango na wanakuwa sehemu ya ligi yetu na timu yetu ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili amependa kufahamu tulikuwa na ligi ya Muungano sasa anapenda kufahamu ni ligi hii itarudishwa? Nijibu hili kwamba jambo hili sisi kama Wizara pia tumeliona. Tumekuwa sasa na mazungumzo kati ya BMT, TFF pamoja na ZFF kuhakikisha kwamba ligi hii inarudishwa.

Mheshimiwa Spika, mwanzoni ilisitishwa kwa sababu Zanzibar ilipata associate membership kwa CAF wakawa wanapeleka timu zao mbili na huku Bara pia wakawa wanapeleka pia timu zao mbili. Lakini kwa afya ya Muungano wetu, kwa afya ya mashirikiano tuliyonayo kama Taifa tumekubaliana na kamati imeshaundwa ligi hii itarudishwa hivi karibuni tunaangalia tu tathmini na gharama kwamba gharama zitakuwaje, lakini itarudishwa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Mheshimiwa Waziri anasema moja ya kigezo cha wachezaji kuteuliwa katika timu ya Taifa ni kupata muda wa kutosha kwa maana ya play time katika ligi za juu kwa maana ya premier na first division. Wachezaji wa Tanzania wanapata vipi nafasi kiasi hicho wakati ligi zetu zimejaa wageni walio wengi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kunipa nafasi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tarimba Abbas kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kwamba hili ni la msingi, lakini sisi tuna limitation ya usajili wa wachezaji wa nje katika timu. Hata wanapocheza wanapoingia uwanjani kocha anazingatia pia kuna uwakilishi wa vijana wetu katika mechi hiyo ya siku hiyo. Tutaendelea kulizingatia na tutaendelee kushauri TFF wahakikishe pamoja na kwamba wamesajili wachezaji kutoka nje kwa limit ile ambayo tumewapa kupitia BMT vijana wetu wanapata nafasi wacheze waoneshe vipaji vyao, ahsante.
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa ya kuuliza swali la nyongeza. Swali linasema: Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu mkakati wa muda mrefu wa kuendeleza vipaji vinavyopatikana kutokana na mashindano ya UMITASHUTA na UMISSETA?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Janeth, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Janeth amependa kufahamu kauli ya Serikali kuhusu kuendeleza vipaji vya vijana wetu vinavyotokana na UMISSETA na UMITASHUMTA.

Mheshimiwa Spika, sisi Wizara yetu kwanza tumshukuru tumshukuru Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, amehakikisha kwamba michezo hii imerudi na ametoa maelekezo kwa Serikali. Tunashirikiana na TAMISEMI, Wizara ya Elimu, pamoja na Wizara yetu, kuhakikisha michezo hii inaendelea, kwa kuwa michezo hii ndiyo inatupatia vipaji vya vijana wetu wanaonzia huko chini kuingia timu za Taifa.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa Wizara yetu inaendelea ku-review kiasi cha fedha kinachotengwa kwa ajili ya UMISSETA na UMITASHUMTA ili michezo hii iwe endelevu. Ahsante. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Lushoto kuna uwanja wa muda mrefu sana lakini uwanja ule unatakiwa ukarabati. Je, nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba inapeleka fedha kwa ajili ya ukarabati uwanja ule?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa michezo ni ajira. Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kuibua, kubaini na kuwahakiki vijana ambao wanataaluma ya michezo hususan Wilaya ya Lushoto hasa Lushoto Vijijini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kunipa nafasi na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Shekilindi swali lake la kwanza amependa kufahamu ni lini Serikali inatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa uwanja huo wa Lushoto lakini viwanja vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika majibu yangu ya msingi nimeeleza kwamba Sera yetu ya michezo imezitaka Serikali kwa ngazi zote Serikali Kuu lakini Serikali za Mitaa kutenga fedha. Ni rahisi sana kama halmashauri zetu, Wakurugenzi pamoja na Waheshimiwa Wabunge na Madiwani tukasimamia kupitia Idara ya Michezo fedha zikatengwa na viwanja hivi vitajengwa na ninyi ni mashahidi tumeanza sisi kwenye wizara bajeti iliyopita tumetenga zaidi ya bilioni 10 kwa ajili ya kujenga viwanja vya kitaifa. Kwa hiyo, naomba nitoe rai tuendelee kutenga fedha kwa Serikali kwa ngazi zote ili tujenge viwanja hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili Mheshimiwa Shekilindi amependa kufahamu ni jinsi gani tunashirikiana na TAMISEMI pia kuhakikisha vipaji vinaibuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wizara tumeshatoa maelekezo kwa ngazi zote na kwa vyama vyetu na mashirikisho, kwamba vipaji vinapoibuliwa vyama na mashirikisho yaweze kushiriki. Naomba nipongeze kwa niaba ya Waziri, Wabunge na Madiwani ambao wamekuwa wakichezesha ligi mbalimbali katika maeneo yao, maana yake wanaibua vipaji. Sisi kama Wizara tunakuja na mtaa kwa mtaa kuhakikisha kwamba tunapofika kwenye lengo la Taifa la Taifa cup tunahakikisha kwamba huko chini vipaji vimeibuliwa. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; kwanza nimpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Pauline Gekul kwa kujibu maswali vizuri. Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunashirikiana vema na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo imetuelekeza kupitia Sanaa, Michezo na Utamaduni tunatengeneza ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitoa maelekezo kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa, Shule za Msingi na Sekondari kote nchini kuhakikisha maeneo yanapimwa na tunapata haTi kufika Disemba, 30; na nimeelekeza kopi ya hati ije Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili niweze kujiridhisha kila shule ya msingi na sekondari imepimwa na kupata hati. Tunafanya hivi ili kuhakikisha maeneo ya shule tunapunguza uvamizi ikiwemo maeneo ya michezo kwa maana ya viwanja vya michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nitumie nafasi hii kuwaagiza Wakurugenzi kufanya kipaumbele kwenye bajeti za Mamlaka za Serikali za Mitaa, kutenga fedha kwa ajili ya kujenga viwanja vya michezo ni moja ya vipaumbele katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza swali la nyongeza. Serikali ina mpango gani kujenga uwanja wa michezo Mkoa wa Simiyu unaoendana na hadhi ya Mkoa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi. Naomba nijibu swali la Mheshimiwa Midimu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mikoa yetu tuna ma-RAS ambao ni wenyeviti wa michezo, lakini kwenye wilaya zetu tuna ma-DAS ambao ni wenyeviti wa michezo, lakini tuna Wakurugenzi wetu tuna Maafisa Michezo kama ambavyo nimejibu kwenye majibu yangu ya msingi kwamba ni jukumu sasa Serikali za Mitaa wakatenga bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili jambo linapaswa lianze haraka ili wananchi ambao wana vipaji vyao viendelee kuibuliwa kwa kucheza katika viwanja ambavyo ni vizuri. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Mkoa wa Simiyu kutenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi huo. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Serikali haijawekeza sana kwenye viwanja vya masumbwi na kupelekea wanandondi kufanya mazoezi kwa kutumia njia za asili ikiwemo matairi. Je, ni lini Serikali itawekeza kujenga maeneo sahihi ambayo wanamasumbwi hao waweze kufanikiwa kama kijana wetu Mwakinyo anavyofanya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mwakagenda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mwakagenda pamoja na Wabunge wengine wote kuhakikisha kwamba mchezo huu wa ngumi unafika mbali. Nimhakikishie kwamba, miongoni mwa maelekezo ambayo tunatoa katika nyanja mbalimbali na katika mashirikisho ni kuhakikisha kwamba miundombinu inajengwa, kwa sababu kila chama cha mchezo kina jukumu kwa mujibu wa sera yetu kuhakikisha vijanja na miundombinu inajengwa. Kwa hiyo, sisi tutaendelea kusimamia kama wizara kuhakikisha kwamba hayo maeneo yanapatikana. (Makofi)
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mhehimiwa Spika, Bunge lako Tukufu lilipitisha fedha kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Michezo Nchini. Sasa nataka kufahamu tu kwamba majukumu makubwa ya fungu hilo ilikuwa ni pamoja na kuunga mkono juhudi zinazoendelea mikoani za ujenzi wa viwanja: Je, ni Shilingi ngapi ambazo Wizara inaweza kuipatia Halmashauri ya Mji wa Geita?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa Tanzania imekuwa haipati matokeo yanayoridhisha inapokwenda kwenye michezo mbalimbali nje ya nchi; na hii inasababishwa na kukosekana kwa mpango na mkakati unaopimika wa kuendeleza michezo nchini: Ni upi mpango wa haraka ambao wizara inao ili kuweza kujikwamua kwenye eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, naomba sasa nijibu maswali ya nyongeza mawili ya Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza Mheshimiwa Kanyasu anapenda kufahamu ni kwamba Bunge hili lilitupitishia fedha kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Michezo na hadi sasa ni shilingi ngapi zimetumika lakini pia kama tunaweza kuwasidia Geita Mji katika ujenzi wa uwanja ule.

Mheshimiwa Spika, tushukuru Bunge hili Tukufu na Mheshimiwa Rais kwa kutupatia fedha hizi, ambazo zimetusaidia sana kwenye Timu za Taifa ambapo mmeona kwa kiasi kikubwa sana wameletea heshima Taifa letu. Sisi kama Wizara tulivyoomba fedha hizi, lengo kubwa lilikuwa ni kujenga viwanja vya kitaifa ambavyo vitasaidia vijana wetu ambao wametoka kwenye ngazi za chini kuweza kucheza kwenye viwanja vizuri. Jukumu hilo tumeanza, lakini na Halmashauri ya Geita hatujaiacha, tumewapa maelekezo mbalimbali ili waandae uwanja huu vizuri.

Mheshimiwa Spika, naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba fedha hizi zitakapokuwa zinatosha baada ya timu za Taifa kuhudumiwa, tuko tayari kuendelea ku- support jitihada hizi za Taifa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili Mheshimiwa Kanyasu anapenda kufahamu ni mkakati gani Wizara yetu tumeandaa kwa ajili ya kuhakikisha tunapata wachezaji wazuri kwa ajili ya kuendeleza michezo katika Taifa letu? Kwanza Bunge hili Tukufu mlitupatia Shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya Chuo cha Malya ambacho kinatoa mafunzo kwa Makocha wetu. Pia Bunge hili Tukufu mlitupitishia fedha zaidi ya Shilingi bilioni mbili kwa ajili ya Academy 56 nchi nzima ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri wa Elimu amejibu hapa na fedha hizi sisi tumetenga.

Mheshimiwa Spika, vile vile tunaendelea kukarabati viwanja saba vya zaidi ya Shilingi bilioni 10 ambavyo tulivitaja hapa vikiwemo vya Mbeya, Dodoma, Arusha na maeneo mengine kuhakikisha kwamba tunaboresha miundombinu na tunawapata wataalam kupitia fedha hizi ambazo mnatutengea.
MHE. DAVID C. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na ninakuomba kwa ridhaa yako kabla ya maswali yangu mawili ya nyongeza nitumie nafasi hii kuwapongeza Serengeti Girls na Tembo Warriors kwa kufika hatua ya robo fainali, lakini pia kuwapongeza Simba Queens ambao leo wanacheza hatua ya nusu fainali na Mamelodi Sundowns na kuwapongeza Simba kuingia hatua ya makundi na kuwaombea Yanga leo dhidi ya Club Africain waweze kushinda na kuingia hatua ya makundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizo nina maswali mawili ya nyongeza. Je, Serikali iko tayari kuona kwamba sehemu ya fedha hizi inatumika pia katika kuboresha mchezo wa riadha ambao unaweza kutusaidia katika kujitangaza kwa umadhubuti katika kushiriki michezo kama vile Tokyo Marathon, New York Marathon, Bostin Marathon na kadhalika?

Swali la pili, kwa muda mrefu mojawapo ya shida katika michezo yetu hasa mchezo wa soka ni kiwango duni cha waamuzi.

Je, Serikali iko tayari kutenga sehemu ya fedha hizi kufanya mafunzo maalum kwa ajili ya waamuzi ili waamuzi wetu kuwajengea uwezo na hivyo kuwawezesha kushiriki katika kuchezesha michezo ya AFCON, World Cup na kadhalika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza Mheshimiwa Chumi amependa kufahamu kama Serikali ipo tayari sasa kutenga sehemu ya fedha hizi kuhakikisha pia wanaweza ku-support riadha. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba sisi kama Wizara tunayo michezo Sita ya kipaumbele ikiwemo riadha. Kwa hiyo, tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ku-support riadha ili iendelee kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, amependa kufahamu kama fedha hizi pia zitatumika katika kuwezesha waamuzi. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu na Watanzania pia kwamba chini ya BMT wameendelea kusimamia kwamba vyama vya michezo waweze kuwaandaa waamuzi. Na niwapongeze TFF wiki hii iliyopita walikuwa na programu ya vijana 30 pale Uwanja wa Taifa wakishirikiana na FIFA kuhakikisha kwamba tunapata waamuzi kwenye michezo hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, michezo sasa ni ajira na Wizara kwa maana ya Serikali ina mpango wa kujenga shule 56 nchini ambazo ni academies kwa ajili ya shughuli za michezo.

Je, ni lini sasa ujenzi wa shule hizi utaanza?

Mheshimiwa Spika, ningependa pia kujua katika shule 56 ambazo ni sports academies zitakazojengwa nchini, ni shule ngapi zitajengwa katika Mkoa wangu wa Tanga? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA SANAA, UTAMADUNI NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Husna Sekiboko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Husna kwanza amependa kufahamu ni lini ujenzi wa shule hizi 56 teule utaanza. Naomba niliarifu Bunge lako tukufu kwamba ujenzi wa shule hizi umeshaanza na tunashukuru Bunge lako tukufu mlitupitishia zaidi shilingi bilioni mbili na sasa zaidi ya shule saba zimeshapitiwa na ujenzi umeanza na unaendelea.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili Mheshimiwa Husna alitaka kufahamu Mkoa wa Tanga katika hizi shule 56 teule za michezo una shule ngapi? Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba takribani Mikoa yote timu ambayo imetoka TAMISEMI, ambayo imetoka Wizarani kwetu na Wizara ya Elimu imeteua shule mbili kwa kila Mkoa, lakini kuna baadhi ya mikoa ina shule tatu kulingana na mazingira ya watu wenye uhitaji, lakini zaidi kila Mikoa ina shule mbili mbili.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Tanga naomba nimtajie shule zake kwamba ni Tanga Technical Secondary School na Nyerere Memorial Secondary School pia katika mwaka huu miongoni mwa shule hizi saba, shule hii ya Tanga tunakwenda kuanza ujenzi maana tunategemea UMITASHUMTA na UMISETA tutahamia huko baada ya kutoka Tabora. Ahsante. (Makofi)
MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jibu zuri: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza; kwa kuwa, Serikali inafahamu fika michezo sanaa na tamaduni ni moja ya suluhu ya kuongeza ajira katika nchi yetu. Sasa Serikali haioni sababu ya kuipa kipaumbele michezo, sanaa, ili waweze kutatua tatizo la ajira kwa watu wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khadija, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa naibu Spika, ahsante. Swali lake la kwanza alipenda kufahamu ni kwa kiasi gani Wizara tunahakikisha kwamba, tunaendelea ku- promote michezo hii ya wtu wenye ulemavu katika maeneo mbalimbali: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yetu inahakikisha na tunashirikiana na vyama mbalimbali, katika miundombinu tunahakikisha watu wenye ulemavu wanapewa kipaumbele, hata katika ujenzi wetu wa shule 56, miongoni mwa shule ambazo tumezitenga zipo za watu wenye ulemavu. Kwa hiyo, tunaendelea kuwashirikisha na kuwajengea miundombinu.
MHE. GEOFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Kwa kuwa tunashida kubwa ya ajira kwa vijana, lakini pia kwa kuwa tunajua kuna vipaji vingi vya vijana kwenye nchi yetu, lakini pia kwa kuwa tunafahamu ziko nchi zimewekeza vya kutosha kwenye vijana kama vile Brazil, Congo DRC, Senegal, Nigeria, Ghana, naomba sasa niulize maswali yangu mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ningependa kujua kwamba kutokana na umuhimu huu ambao nimeusema, Wizara inaweza ikatengeneza utaratibu kwa kuanza kuweka bajeti kidogo ya kuweza kusaidia Halmashauri za Miji Midogo ambayo haina uwezo wa kibajeti kuweza kuendeleza viwanja ambavyo tayari vipo kwenye maeneo yale? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tunafahamu kwamba kuna juhudi kubwa zinafanywa na watu binafsi kwenye kuendeleza vijana kupitia shule mbalimbali za soka. Je, Serikali inaona ni muhimu sasa kuweza kusaidia vituo vya kulelea vijana na hasa ukuzaji wa vipaji vya soka na michezo mingine ili tuweze kupata vijana ambao wameandaliwa vizuri kwa ajili ya timu ya Taifa na kuweza kupata ajira nje ya nchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwambe, Mbunge wa Masasi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza alipenda kufahamu kama Serikali tupo tayari ku-support halmashauri ambazo bajeti zao ni chache na wasingeweza kufanya kazi hii.

Mheshimiwa Spika, katika majibu yangu ya msingi nimesema kwamba jukumu hili ni la Serikali Kuu, lakini pia Serikali za mitaa. Naomba nipongeze Halmashauri ya Masasi wao wameshaanza kuzungusha uzio katika uwanja ule, lakini pia sisi kwa upande wa Wizara pia tumeanza kujenga baadhi ya viwanja na katika mwaka huu wa bajeti, tulitenga viwanja zaidi ya saba. Pale bajeti ambapo itaruhusu sisi tutaendelea ku-support.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili alitaka kufahamu ni kwa kiasi gani tunaweza tuka-support vituo vya kukuza vipaji (academies).

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara tunaandaa mazingira wezeshi kuhakikisha hizi academy zinafanya vizuri na mpaka sasa tuna academies binafsi zaidi ya 84. Kwa hiyo, sisi Wizara tutaendelea ku-support. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la msingi.

Kwa kuwa shule nyingi sana za sekondari, za msingi na vyuo zina viwanja vibovu sana na Mheshimiwa Waziri amesema kwamba kuna baadhi ya halmashauri tayari zimeanza kutenga hizo fedha. Je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na jambo hilo kwa sababu watoto wetu wanakosa haki yao ya msingi ya kutengeneza vipaji vyao?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara na kama Serikali tulishatoa kauli kwamba katika shule zetu tuhakikishe tuna miundombinu ya michezo. Hivyo nitoe rai kwa halmashauri zetu, vyuo na maeneo ambako vijana wetu wanahitaji miundombinu hiyo waendelee kutenga, lakini wavitunze na waviendeleze.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, wakati Naibu Waziri anajibu maswali yake anaonesha jukumu kuu la Serikali pamoja na Serikali za Mitaa ni kujenga, kuhakikisha kwamba viwanja vinajengwa, lakini kuna halmashauri ambazo kwa mwaka mapato ya ndani hayafiki hata shilingi bilioni moja. Hapo ametutajia mfano Halmashauri ya Geita ambayo inapata mrabaha tu shilingi bilioni sita, hao wana uwezo wa kujenga.

Ninataka nijue, ni nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha zile halmashauri ambazo hazina uwezo zinajengewa viwanja walau vyenye hadhi ya kuhodhi ligi ya mkoa?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru, naomba nijibu swali moja la Mheshimiwa Esther, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba suala la michezo ni hitaji la wananchi wetu na tunafahamu kwamba vipaumbele vyetu katika nchi ni pamoja na kuhakikisha magonjwa yasiyoambukiza yanaweza kupigwa vita na wananchi wanakuwa salama. Pamoja na kwamba bajeti zetu hazitoshi katika halmashauri, nitoe rai kwa halmashauri zote kutenga fedha hizi kwa kuwa tusipotenga fedha hizi maana yake hatutekelezi sera hii ya maendeleo ya michezo.

Kwa hiyo, hata kama bajeti zetu ni ndogo tutenge, kwa mfano Halmashauri hii ya Masasi, Mheshimiwa Mbunge pia ametenga sehemu ya Mfuko wa Jimbo kuhakikisha ana- support jitihada za halmashauri, kwa hiyo, tuendelee kutenga fedha.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi ni moja kati ya viwanja kongwe nchini ambacho kiko katika Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Spika, je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha uwanja huo ili na wenyewe uweze kutumika katika michezo?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Mwaifunga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara yetu pia tunapojenga viwanja hivi tunaangalia na ukanda, lakini pia katika jitihada za Serikali tumehakikisha kwenye vile vipaumbele vyetu kwa upande wa academies tulizozianza, Tabora tulianza nao.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Hawa naomba nipokee ombi hili kwamba tutaendelea kutenga fedha kama ambavyo tumetenga kwenye viwanja saba vya mwaka huu, zaidi ya shilingi bilioni 10 tumeanza kazi, kwa hiyo tutawafikia.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru Serikali kwa majibu mazuri ya kuihakikishia Halmashauri au Wilaya ya Kibiti kupata Mahakama ya Wilaya. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa sasa hivi Mahakama hiyo iko kwenye jengo la Mahakama ya Mwanzo ambalo limechakaa. Je, Serikali ina mpango gani kulitumia au kulifanya ukarabati jengo hilo ambalo litabaki kutumika kama Mahakama ya mwanzo?

Swali la pili; Mkoa wa Pwani una Mahakama za Mwanzo 21, kati ya hizo zipo ambazo zimechakaa na nyingine zimebomoka babisa ikiwemo ya Kibaha Vijijini pale Kata ya Ruvu na Kata ya Magindu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuzijenga hizi zilizobomoka na kuzifanyia ukarabati zile ambazo zimechakaa.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika,
ninakushukuru, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Michael Mbunge wa Kibaha Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nipende kufahamu endapo tutajenga Mahakama hii ya Kibiti hilo jengo ambalo sasa linatumika kama tutalikarabati. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jengo hilo litaendelea kutumika na Mahakama ya Mwanzo kwa kuwa saa hizi wametuhifadhi Mahakama ya Wilaya, kwa hiyo tutalikarabati.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anapenda kufahamu katika Mkoa wa Pwani Mahakama ya Mwanzo hizi mbili ambazo amezitaja. Mahakama yetu imeweka mpango kabambe wa kuhakikisha tunakarabati Mahakama zote ambazo zimechakaa, katika Mkoa wake wa Pwani tunakwenda kukarabati Mahakama 19 pamoja na hizi mbili ambazo amezitaja.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kuzijenga Mahakama za Mwanzo za West Meru Mkwaranga na Ngerenanyuki ambazo ziliachwa tu zikaharibika kabisa sasa hivi yamebaki magofu?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru, naomba nijibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Pallangyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mpango wetu wa ujenzi na ikarabati wa mahakama katika mwaka huu wa fedha tunategemea kukarabati na kujenga Mahakama 60 za mwanzo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika Mkoa wake pia Arumeru tumeweka Mahakama za kukarabati tutampatia list ataona Mahakama zake kama zinahitaji kukarabatiwa.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Sheria iko wazi kuzuia mahusiano na mapenzi ya jinsia moja, lakini tunaona kwenye vyombo vya habari watu wakitangaza na kujinasibu kujihusisha na mapenzi ya jinsia moja.

Je, ni hatua kiasi gani zimefanyika kufikishwa Mahakamani ili tuweze kuzibiti kwa mujibu wa sheria? (Makofi)

Swali langu la pili, licha ya kuwepo kwa Sheria bado tumeona utekelezaji wake, pengine utekelezaji ndiyo umesababisha haya tunayoyasema.

Je, ni lini Serikali italeta mabadiliko ya sheria ili kila anayejihusisha, mwenye dalili na mwenye kufikiria aweze

kuchukuliwa hatua ili tuweze kulinda maadili ya nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Theonest kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge amependa kufahamu kwamba makosa hayo yanapojitokeza na watu wakijinasibu hadharani kwenye vyombo kama hatua zimekuwa zikichukuliwa? Hatua zimekuwa zikichukuliwa na ninyi ni mashahidi kwenye Bunge hili tumekuwa tukikemea jambo hili, nitoe rai kwa jamii kwamba jambo hili si la Serikali peke yake ni la jamii kwa umoja wetu ndiyo maana pale zinapokuwa zimebainika tumekuwa tukichukua hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge anahitaji kujua kama tunaweza kufanya marekebisho ya sheria hizi? Sheria hizi zinafanya kazi kuhakikisha kwamba wale wanaobaninika wanachukuliwa hatua na ninyi ni mashahidi ndugu zangu hivi karibuni mahakama zetu zimetoa hukumu kwa watu ambao wamebainika wamefanya hivyo na wamekiri na wamefungwa miaka zaidi ya thelathini. Kwa hiyo, ni jukumu letu sote. Hata hivyo, pale ambapo utafiti utakuwa umefanyika Mheshimiwa Spika alielekeza kwamba utafiti wa kina ufanyike ili matendo haya yakibainika basi tuwe na kauli ya pamoja. Wakati huo ukifika kama marekebisho ya sheria yatahitajika Serikali ipo tayari.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Niabu Waziri kwa majibu. Namwona Mheshimiwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mheshimiwa Nape.

WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kuongeza katika majibu yake mazuri.

Kwanza, hakuna matangazo ya mapenzi ya jinsia moja kwenye main media ambayo yanaruhusiwa na Serikali iko very strictly kwenye hili. Tulikuwa na chanagamoto kwenye online media ambayo mpaka sasa hivi jumla ya tovuti 334, akaunti za Facebook 361, Instagram 168, Twitter 12 na vikoa vya gay zaidi ya 2,456 vimefungiwa kwa sababu ya hatua hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na hatua ambazo Serikali inachukua kufungia baadhi ya hizi online platforms lakini nadhani jambo hili bado liwe ni jukumu la jamii kuchukua hatua kuanzia kwenye familia na kuendelea sasa kwenye maeneo mengine. Nashukuru. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri kabisa ya Serikali, ninashukuru sana kwa uamuzi huu uliofikiwa sasa hivi, Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi kwamba kuna mkanganyiko mkubwa hasa zaidi kwenye Sheria hizi mbili za Sheria ya Ndoa na Sheria ya Mtoto. Mtoto anatambulika chini ya miaka 18 lakini ndoa inaruhusiwa kufungwa akiwa na miaka 14. Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba tunaiomba Serikali sasa ilete kwa haraka sasa sheria hii ili Wabunge tuweze kuipitia na kuifanyia marekebisho makubwa.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya pili ni kwamba kumekuwa na usumbufu mkubwa sana kwa Wajane na Wagane hasa wanapofuatilia masuala ya mirathi na yenyewe hapa kwenye majibu ya Serikali wamasema watahakikisha wanaleta kwenye Bunge hili, tunataka tufahamu wakati mahususi kwa sababu sheria hii imepitwa na wakati ili iweze kujadiliwa na Wabunge na kupata matokeo mazuri. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika,
nakushukuru, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cecil Mwambe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nakubliana nae kwamba Sheria hii ya Ndoa kuna baadhi ya vifungu ambavyo kwa kweli vimekuwa vikilalamikiwa hasa kile kifungu cha 13 na kifungu cha 17 ambazo zimetofautina katika umri wa mtoto wa kike kuolewa, lakini wakati mwingine Mahakama imekuwa ikitoa ruhusa hiyo pale wazazi wanapokuwa wameridhia, ndiyo maana Wizara tumeshakamilisha mchakato huu sasa tuwaleteeni katika Bunge hili tuweze kuamua na umri ambao utakuwa umependekezwa tutauona katika Muswada ambao tutauleta katika Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameeleza kuhusu Wagane na Wajane ambao wamekuwa wakisumbuliwa katika masuala ya mirathi. Nimeeleza katika Sheria hizi ambazo zinasimamia mirathi ya kidini lakini pia wale ambao wanatumia Sheria hii ya Indian Succession nimeeleza kwamba taratibu hizi zipo lakini bado kuna malalamiko ndiyo maana Tume yetu ya Kurekebisha Sheria tumeiagiza pia ifanye utafiti watuletee. Katika Bunge hili tunategemea kuleta marekebisho ya Sheria zaidi ya 27.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naishukuru Serikali tunategemea kuletewa Muswada, lakini nina maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; sheria hizi zinazohusu ukiukwaji wa haki za kibinadamu ikiwepo ndoa za utotoni, ukeketaji, ubakaji, ulawiti, ukatili wa kijinsia pamoja na kutungiwa sheria kali ikiwepo miaka thelathini jela kwa kosa la ubakaji, lakini matendo haya yamekuwa yakiongezeka kwa kasi kubwa. Sababu kubwa ni kutoa mwanya wa makosa hayo kusuluhishwa kijamii. Je, sasa Serikali inasimamiaje sheria hizi kuhakikisha kwamba inaondoa ukiukwaji wa haki za kibinadamu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Sheria ya Ndoa inasemaje kuhusu wanawake kumiliki mali? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rahhi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge ameeleza vyema kwamba tatizo siyo sheria, tatizo ni sisi wanajamii kutokuwafikisha hao wahalifu kwenye vyombo vya dola. Nitoe rai kwa wanajamii kwamba makosa haya yanaumiza Watanzania wenzetu, Watoto, wasiyavumilie kwa kuyasuluhisha nyumbani na kuisha, wapeleke kwenye vyombo vinavyohusika hatua zichukuliwe kwa mujibu wa sheria kama ambavyo sheria zetu zinataka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili Mheshimiwa Mbunge amehitaji kufahamu Sheria yetu ya Ndoa inasemaje katika umiliki wa mali. Sheria hii ya Ndoa siyo kwamba ni mbaya kiasi hiki ambavyo watu wanafikiria, ina vifungu zaidi ya 167, ni vizuri kabisa, vichache tu ndiyo vina usumbufu Kifungu cha 13 na 17. Sheria yetu hii imesema katika Kifungu kile cha 56 wanandoa wote wana haki ya kumiliki mali, iwe ni mke iwe ni mume wote wana haki sawa. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mahakama ilishatoa uamuzi kuhusu suala la umri la watoto wadogo kuolewa Tanzania. Serikali haioni kuendelea kukusanya maoni ni kukiuka amri ya Mahakama?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali na Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria amesema vizuri kwamba, tulishaleta kwenye Bunge lako hili Tukufu na nimesema kwenye majibu yetu ya msingi, kwamba ni Bunge hili na Kamati hii ilitutaka turudi kwa wananchi ili tupate wigo mpana wa kuwahusisha Watanzania katika hili. Kwa sisi hatuna tatizo na niwakaribishe Waheshimiwa Wabunge kesho wenye nafasi mje tunamaliza hayo majadiliano katika Hoteli ya Morena kesho Saa Saba Mchana, tukishakamilisha tutaleta sheria hii Bungeni. Ilikuwa ni agizo la Bunge siyo la kwetu.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na utayari wa Serikali kufanya marekebisho ya Sheria ya Ndoa lakini bado kuna Sheria za Kimila kandamizi kwenye mirathi. Je, ni kwa nini sasa Serikali isione haja ya kupitia upya Sheria za Kimila ili kuondoa ukatili wa kijinsia na ukandamizaji wa wanawake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kunipa nafasi nijibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi kwamba sheria zetu za kimila, tuna sheria tatu za mirathi, tuna ya kidini Sheria ya Kiislamu Sheria ya Kimila na Indian Succession Act. Hizi sheria zote zimekuwa zikizungumzia jinsi gani watu wananweza kupata haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa sheria ambazo tumezisema katika Bunge hili kwamba tunazifanyia marekebisho ni pamoja na sheria hizi za mirathi za kimila ili Watanzania wote wapate haki zao. Kwa sababu katika sheria ambayo Mheshimiwa Mbunge ame-refer wanawake wengi hawapati haki zao, wanakuwa katika marriage lakini watoto wanapewa mali wakati wale akina mama ambao wamezaa wale watoto wanakosa haki. Kwa hiyo, tunakuja na marekebisho ya sheria hizo. (Makofi)
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na ahsante kwa majibu ya Serikali.

Kwa kuwa, ufanisi wa Mabaraza umekuwa mdogo sana kwa sababu hayapo kila Wilaya, ukilinganisha kwa mfano Itilima wanapata huduma Maswa, Meatu wanapata huduma Maswa na tumefanya wanachi kuingia gharama kubwa bila sababu za msingi. Ukisoma Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Ibara ya 74(1) ukurasa wa 179, imeeleza kwamba Mabaraza haya sasa yahamishiwe kwenye Muhimili wa Mahakama.

Je, ni lini Serikali itaanza mchakato huo na kuukamilisha mapema?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ninakushukuru na naomba nijbu swali moja la Mheshimiwa Simon Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninampongeza Mheshimiwa Simon kwa kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Wizara yetu ya Katiba na Sheria pamoja na Wizara ya Ardhi pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama na mfumo mzima wa Mahakama wako kwenye hatua za mwisho za kukamilisha mjadala huu wa kuhamishia Mabaraza haya kwenye Muhimili wa Mahakama kama ambavyo Ilani ya Chama cha Mapinduzi imeeleza. Ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. pamoja na majibu ya Serikali, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwenye mapendekezo ambayo ameyataja hapo sikuona suala zima la elimu kwa raia, kwa wananchi, kwa maana Katiba si mali ya wanasiasa pekee ni mali ya wananchi. Je, Serikali imejipangaje kuanzisha elimu japo kwa Katiba hii iliyopo ya mwaka 1977 ambayo wananchi wengi hawaifahamu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; wakati wa rasimu ya Mheshimiwa Warioba, mwaka 2012, mpaka sasa ni takribani miaka kumi na moja, wapo Watanzania ambao wakati ule walikuwa na umri mdogo na sasa wametimiza miaka 18.

Je, Serikali katika mapendekezo hayo itazingatia kwenda upya kutafuta maoni ya wananchi ili kujenga wigo mkubwa wa ukusanyaji wa maoni?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza kuhusu elimu kwamba, itolewe ya Katiba iliyopo. Serikali tumejipanga na ndio maana katika bajeti yetu ambayo tuliileta kwenu Waheshimiwa Wabunge tumeweka pia bajeti kwa kazi hiyo. Kwa hiyo Serikali tutatoa elimu ya Katiba iliyopo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, lakini pia Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984. Katiba hizi zote tutapeleka elimu kwa wananchi ili wazifahamu kabla mchakato huu haujaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, amependa kufahamu pia kama wananchi ambao kipindi kile cha rasimu ya Mheshimiwa Warioba hawakushiriki kutoa maoni yao kwa sababu ya umri, kama kipindi hiki watashirikishwa: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wote wa Tanzania watashirikishwa. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuona hili, ndio maana sasa mchakato huu unaanza ili na wale ambao hawakupata nafasi ya kutoa maoni yao basi na wao waweze kutoa maoni yao.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya Mahakama za Mwanzo katika Tarafa za Mwimbi, Kasanga na Mwazye na Mambwe Nkoswe ni chakavu kwelikweli. Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya ukarabati wakati ikiwa inafikiria kujenga Mahakama mpya za Mwanzo?

Swali la pili; kwa kuwa Tarafa ya Mambwe Nkoswe ambayo ni kilometa 150 kwenda Makao Makuu ya Wilaya haina kabisa hata Mahakama ya Mwanzo. Je, Serikali iko tayari kwa uharaka kuhakikisha kwamba tunajengewa Mahakama ya Mwanzo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Josephat Kandege, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu wa fedha Mahakama imetenga fedha kwa ajili ya kujenga Mahakama katika Kata hii ya Kasanga ambayo ni hitaji la Mheshimiwa Mbunge. Kwa Tarafa ambayo ameitaja katika swali la pili, naomba nimuarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba Mahakama itaendelea kutenga fedha kukamilisha Mahakama za Mwanzo ambazo hazijajengwa katika maeneo ambayo kuna uhitaji, ahsante.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakama ya Wilaya ya Kiteto ni ya zamani kidogo na majengo yamechakaa. Kwa jibu la uhakika kabisa, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya kwenye Jimbo la Kiteto?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Edward Olelekaita, Mbunge wa Kiteto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mpango wa Mahakama, Mahakama ya Wilaya ya Kiteto itajengwa katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Serikali ilituahidi kujenga Mahakama ya Mwanzo Tarafa ya Namanyere, ninapenda kujua utaratibu huo umefikia wapi.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka ujao wa fedha wa 2023/2024 kwa bajeti yetu ambayo tumepitisha tunakwenda kujenga Mahakama katika Kata ya Namanyere na katika Wilaya ya Nkasi.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na ninapongeza kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, ninaomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuunda hii Tume ya Hakijinai lakini moja kati ya mambo ya msingi ambayo Hakijinai itakwenda kuyafuatilia na kuyaona ni kuhakikisha kwamba huduma za kimahakama kwa maana ya huduma za kisheria kwa wananchi zinasogezwa.

Swali la kwanza, Kata ya Mwakipoya, Masanga, Lagana, Bunambiyu na Mwasuge ni Kata ambazo ziko pembezoni na ziko mbali na maeneo ya huduma ya kisheria. Sasa ni nini mpango wa Serikali walau wa kusogeza huduma hizi kujenga katika Kata hizi muhimu hizi Nne? (Makofi)

Swali la pili, huduma hizi za kisheria ni za muhimu sana na Halmashauri ama Wilaya ya Kishapu haina Mahakama ya Wilaya. Ni lini Serikali inakwenda kujenga Mahakama ya Wilaya katika Wilaya ya Kishapu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika,
nakushukuru kwa kunipa nafasi nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Butondo, Mbunge wa Kishapu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza Mheshimiwa Mbunge amependa kufahamu mpango wa Serikali katika kujenga Mahakama katika kata ambazo amezitaja. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Butondo kwamba tumeshaanza kama Serikali, na mwaka huu wa fedha tumetenga Shilingi bilioni 57 kwa ajili ya kujenga Mahakama 60 za mwanzo nchini. Kwa hiyo, kata zake alizozitaja Mhehsimiwa Butondo zitafikiwa.

Mheshimiwa Spika, swali lake pili ametaka kufahamu kama tuna mpango wa kujenga Mahakama katika Wilaya ya Kishapu. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pia, katika mwaka huu wa fedha, bajeti hii ambayo tulileta katika Bunge hili, kati ya Mahakama 24 za Wilaya ambazo tunazijenga kwa zaidi ya shilingi bilioni 31 na Mahakama ya Kishapu ipo, kwa hiyo itajengwa. (Makofi)
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nashukuru kwa kuianzisha mahakama hiyo. Kwa kuwa Mahakama ya Wilaya ya Nyasa inatumia majengo ya watu binafsi ambao pia wanaweza kuvunja sheria na kutakiwa kushtakiwa katika Mahakama hii;

Je, Serikali haioni kuwa kwa kufanya hivyo inaweza kuwafanya wadau wengine kutokuwa na Imani na Mahakama katika kutoa haki?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Mahakama za mwanzo za Tingi na Litui ni chakavu sana.

Je, ni nini mpango wa Serikali katika kuboresha Mahakama hizi?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru naomba sasa nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stella kama alivyouliza. Swali lake la kwanza, anasema jengo hili la Mahakama ya Wilaya liko katika majengo ya watu binafsi, na anapata wasiwasi kama Mahakama inaweza ikatenda haki pale ambapo mtu huyu ambako tumepanga kwake ana jambo na Mahakama.

Mheshimiwa Spika, nikuhakikishie kwamba muhimili wetu wa Mahakama umeona jambo hili, ndiyo maana tumetenga fedha ili kuhakikisha mwaka huu wa fedha tunajenga Mahakama takribani 24 za Wilaya. Kwa hiyo sisi tutaipa kipaumbele Mahakama hii, na kwa kuwa kazi imeshaanza Mheshimiwa Manyanya awe na imani tu kwamba jengo hili litakamilika ili pasiwepo na wasiwasi wowote, japo Mahakama siku zote inatenda haki.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili amependa kufahamu, kwamba hizi Mahakama za kata ambazo zimetajwa zitajengwa lini na kwamba zimechakaa sana. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, Mahakama yetu ya Tanzania imeliona jambo hili, na ndiyo maana katika mwaka huu wa fedha tumetenga ujenzi wa Mahakama 60 kote nchini. Mahakama inafanya tathmini kujua kata zipi zipo mbali, na mpango wa Mahakama ni kujenga Mahakama katika maeneo ya tarafa ili kuhakikisha kwamba tunatoa huduma. Na taratibu tutaendelea kufikia kama bajeti utaruhusu kwenye hizo kata ambazo uhitaji umeonekana. Ahsante.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali inaendelea kujenga majengo mapya katika maeneo mbalimbali.

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama katika Wilaya ya Mbinga na Songea?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha nimesema kwamba tuna Mahakama 24 tumeziitenga kuzijenga na Wilaya yake ni miongozni mwa wilaya hizo mabazo tutajengea Mahakama. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Mahakama ya Mwanzo ya Usanda katika Wilaya ya Shinyanga imechakaa. Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa Mahakama hiyo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mnzava, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wetu wa Shinyanga tunakwenda kujenga katika mwaka huu wa fedha katika Tarafa ya Majengo, Kata ya Malunga naomba ni-check na Mheshimiwa Dkt. Mnzava ili tuone kwamba Mahakama hiyo ambayo imechakaa tuweze kuingiza kwenye mpango unaofuata wa Mahakama ya ujenzi. Ahsante.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kuniruhusu niulize swali la nyongeza. Wilaya ya Uyui ni mpya na hatuna Mahakama, tunatumia chumba kidogo sana; je, lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Uyui?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru na naomba nijibu swali la Mheshimiwa Maige, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mpango wetu wa kujenga Mahakama za Wilaya ni pamoja na kukarabati ambazo ni chakavu, naomba nipokee Mahakama hii ya Uyui nita-check na Mheshimiwa Mbunge tuone tuiweke kwenye mpango ili tuweze kukarabati pia.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Tarafa ya Heru Juu iliyopo katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu haina Mahakama, inafanyia kazi katika Ofisi ya Mtendaji. Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama katika Tarafa ya Heru Juu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Genzabuke, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mpango wetu wa kujenga Mahakama 60 kote nchini katika bajeti ya mwaka huu, ambayo mlitupitishia, Tarafa ya Heru Juu, Kata ya Heru Juu iko katika list hiyo Mheshimiwa Mbunge tunakwenda kujenga mwaka huu wa fedha. (Makofi)

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa muda mrefu imekuwa na mpango wa kujenga Mahakama ya Mwanzo Kata ya Izigo, Wilaya ya Muleba, ningependa kujua utekelezaji wa ujenzi wa Mahakama hiyo umefikia wapi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru na naomba nijibu swali la Mheshimiwa Oliver Semuguruka, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wetu wa Kagera katika Wilaya ya Muleba Kata hii ya Izigo, Tarafa ya Izigo iko kwenye mpango wa mwaka huu, tunakwenda kujenga mwaka huu Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, Mahakama ya Mwanzo ya Machame ilisimamishwa kwa kipindi kirefu kutokana na uchakavu wa majengo, lakini kwa kushirikiana na wadau tumejenga, tumefanya ukarabati wa Mahakama hiyo ya Mwanzo ya Machame na imekamilika na jengo liko pale.

Je, ni lini sasa mtapeleka Hakimu pale ili aweze kuanza kutoa huduma?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru na naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Saashisha, amechangia katika Mfuko wake wa Jimbo kuhakikisha lile jengo la Mahakama pale Hai – Machame linakarabatiwa, lakini tatizo tulilonalo pale lile jengo bado lina crack nyingi, Mheshimiwa anafahamu hilo.

Mheshimiwa Spika, katika mpango wetu wa Mahakama tumetenga fedha kwenye Kata hiyo ya Machame tunakwenda kujenga eneo lingine. Ninamuhaidi Mheshimiwa Mbunge tutakwenda pale Hai – Machame tuone hilo eneo ambalo lina-disputes hilo ambalo jengo limechakaa na pale ambako tunataka kujenga tutafikia consensus wapi tujenge, ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali na hatua hiyo ya kuanza ujenzi. Mimi nina swali moja tu.

Mheshimiwa Spika, katika Tarafa ya Nambisi kuna Mahakama chakavu katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu. Je, utaratibu wa Serikali ukoje wa kukarabati majengo ya Mahakama katika Tarafa zetu nchini?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa pongezi hizo.

Mheshimiwa Spika, mhimili wetu wa Mahakama una mpango wa miaka mitano wa kukarabati na kujenga majengo ya Mahakama kote nchini na katika mpango huu Mtendaji Mkuu wa Mahakama akishirikiana na Watendaji wa Mikoa wanafanya wanafanya utafiti katika Tarafa zote nchini zaidi ya Tarafa 500 na Kata zaidi ya 3,000 kuona ni wapi ambapo kuna mashauri mengi na umbali, tafiti hii tutakapokamilisha tutakuja sasa na list ya kwamba wapi tuanze.

Mheshimiwa Spika, ninafahamu kwamba hata Nambisi ambako Mheshimiwa Mbunge amepataja kuna uhitaji naomba avute subira tuweze kukamilisha tafiti hii halafu tutamwambia kama hapo tutakwenda kujenga. (Makofi)

MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa juhudi kubwa za Serikali kwenda kutujengea Mahakama ya Wilaya kule Nachingwea. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kuna upungufu mkubwa wa Watumishi katika Idara ya Mahakama Wilaya ya Nachingwea; je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza watumishi kwa ajili ya kuboresha ufanisi wa kazi? (Makofi)

Swali la pili, kwa kuwa Hakimu mmoja anahangaika kuhudumia Mahakama ya Mwanzo zaidi ya tano, lakini fedha za kuhudumia shughuli za Mahakama hazitoshi; je, Serikali ina mkakati gani kuongeza fedha kila mwezi kwa ajili ya shughuli za Mahakama? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru. naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ungele kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ninakiri ni kweli tuna upungufu wa watumishi katika Muhimili wetu wa Mahakama kama ambavyo upungufu huu upo katika Serikali kwa maeneo mbalimbali. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekuwa akituongezea watumishi katika Muhimili wetu wa Mahakama, na ninyi ni mashahidi ndugu zangu ni majuzi tu ametuteulia Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu na kadhalika, tunaendelea kuomba kupeleka vibali kwa ajili ya nyongeza ya watumishi.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Nachingwea ni kweli wana upungufu wa watumishi. Primary Court (PC) ambazo zina Mahakimu ni tatu, Primary Court ambazo zinahudumiwa na hao Mahakimu watatu ni watano. Mheshimiwa Mbunge nikuhaidi kwamba tutaendelea kuwasiliana ndani ya Serikali kuongeza Mahakimu katika Mahakama hizo ili huduma iweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anazunguzia suala la nyongeza ya fedha, kwamba hawa watumishi wanapokuwa wanatoka maeneo hayo kuhudumia Mahakama zile ambazo inabidi waende, kwa kuwa Mahakimu hawajafika wanahitaji fedha kwa ajili ya kuhudimia.

Mheshimiwa Spika, nishukuru Bunge lako Tukufu, nimshukuru Mheshimiwa Rais kwamba mhimili wa Mahakama umekuwa ukiongezewa fedha. Mwaka huu ambao bajeti hii tunayoendelea nayo OC ya Mahakama ilipanda kutoka bilioni 60 mpaka bilioni 70, maana yake tunayo nyongeza ya zaidi ya bilioni 11. Kwa hiyo, tuwashukuru kwamba mmetuongezea na sisi tutaendelea kupeleka hizo fedha za OC ili Mahakimu hawa waweze kuhudumia maeneo ambako wanakwenda kuhudumia. Ahsante.(Makofi)
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Tarafa ya Ruponda katika Wilaya ya Nachingwea haina Jengo la Mahakama ya Mwanzo; je, ni lini Serikali itajenga Jengo la Mahakama ya Mwanzo kwenye Tarafa hii ya Ruponda iliyoko Makao Makuu ambayo yako kwenye Kata ya Ruponda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naomba sasa nijibu swali Mheshimiwa Amandus Chinguile, Mbunge wa Nachingwea, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Tarafa hii ya Ruponda ambako Mheshimiwa Mbunge ametamka, iko kwenye mpango wetu wa bajeti. Kwenye zile Mahakama 60 tunakwenda kujenga Mheshimiwa Mbunge, na tunafahamu ina umbali wa zaidi ya kilometa 14 kufuata huduma eneo lingine. Kwa hiyo, liko kwenye mpango tumeweka. Ahsante. (Makofi)
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, Wilayani Rungwe, Kata ya Kiwira ina Mahakama ya Mwanzo. Mahakama hiyo ni ya muda mrefu sana haijafanyiwa ukarabati, ukizingatia Mahakama hiyo inategemewa na Kata ya Ndanto, Isongole, Kinyala, Swaya, Kyimo na Kiwira yenyewe.

Je, ni lini Serikali itakwenda kufanya ukarabati wa Mahakama hiyo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Suma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, awali nilisema kwamba tuna mpango wa kukarabati majengo ya Mahakama kote nchini. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwamba ameridhia wenzetu wa World Bank wametupa zaidi ya dola milioni 90, zaidi ya bilioni 200 kuhakikisha tunaboresha miundombinu ya Mahakama kote nchini. Nikuhaidi Mheshimiwa Mbunge baada ya tafiti yetu kufanyika kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama akishirikiana na Watendaji wa Mikoa kuona maeneo ambapo pamechakaa zaidi tutakuja na mpango huu ili tuingize na hayo maeneo ambayo yamechakaa tuyaboreshe, ahsante. (Makofi)
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Majengo ya Mahakama ya Mwanzo katika Jimbo la Mwibara yamechakaa kabisa. Je, ni lini Serikali itajenga upya majengo hayo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimetangulia kusema kwamba fedha hizi ambazo tumezipata haziishi kujenga Mahakama za Mwanzo ni pamoja na za Wilaya, lakini tunajenga pia Integrated Justice Centers kwenye Mikoa, kujenga Mahakama Jumuishi kuanzia Mahakama ya Mwanzo ya Wilaya, Mkoa mpaka ya juu. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika mpango huu pia tutakufikia. Ahsante. (Makofi)
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Wananchi wa Tarafa ya Terati pamoja na Tarafa za jirani ikiwemo Mji mdogo wa Mererani wamekuwa wakitembea umbali mrefu kufuata huduma za Mahakama. Je, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo katika eneo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Regina Qwaray, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Manyara na katika Wilaya ya Simanjiro tunakwenda kujenga Mahakama hiyo ya Terati, lakini siyo hapo tu pia tuna Mahakama ya Orkesumet, Mheshimiwa Regina umekuwa ukilifuatilia hili, tunaanza ujenzi mwaka huu. Ahsante.(Makofi)
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu ya Serikali ni mazuri na imeonesha kwamba sheria ipo, lakini ukweli ni kwamba utekelezaji wa sheria hii umekuwa ni hafifu sana. Pia kama hivyo ndivyo, Watanzania wengi wamekuwa wakiathirika na utekelezaji huu hafifu wa hii sheria, kitu ambacho kinawafanya waathirike kisaikolojia, kijamii na hata kiuchumi. Vilevile wanapotoka na kuja mtaani baadaye watu hawa wanakua wamepoteza uelekeo sana lakini tunajua utekelezaji huu hafifu wa hii Sheria umeipa mzigo mkubwa sana Serikali kwa kuwahudumia watu ambao wanakaa muda mrefu rumande. Kitu ambacho tulivyofanya ziara mbalimbali tumeona kabisa kuna watuhumiwa wengi…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Neema, uliza swali.

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wananchi wengi wako gerezani kwa zaidi ya miaka 15. Swali la kwanza; je, Serikali ina mkakati gani wa kuwalipa fidia watuhumiwa wote waliokaa mahabusu muda mrefu na kushinda kesi hizo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, nataka kufahamu ni nini kauli ya Serikali katika kufuta kesi zote za watuhumiwa waliokaa zaidi ya miaka mitano mahabusu?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Naomba sasa nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Neema Gerald, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sio kweli kwamba haya tunayoongea hapa hayatekelezeki, ndio maana ukiangalia kwenye takwimu zetu za masijala za mahakama hadi jana tarehe 29/5/2023 mashauri ni 1,863 lakini backlogs ambazo hazijafanyiwa kazi ni asilimia nne tu. Hapa maana yake ni nini? Maana yake Mahakama imekuwa ikizisikiliza kesi hizi na zimekuwa zikihukumiwa na kuondoka na sasa katika mahakama zetu hakuna kesi ambayo mtuhumiwa yuko mahabusu mpaka sasa zaidi ya miaka mitano hajahudumiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumshukuru Mheshimiwa Rais, amekuwa akiboresha mahakama zetu, amekuwa akiteua Majaji, amekuwa akitoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama Kuu na mwaka huu wa fedha tunakwenda kujenga Mahakama za Mikoa zaidi ya 14 ili Majaji hawa wakasikilize kesi hizi. Kwa hiyo, naomba nilihakikishie Bunge lako tukufu kwamba kwenye Mahakama kesi hizi zinasikilizwa na kasi imeongezeka ndio maana backlogs zimebaki asilimia nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, anataka kufahamu kama watu hawa waliokaa zaidi ya miaka mitano wanaweza wakafidiwa. Taratibu za kisheria na principles za kesi kwamba pale ambapo unaona kwamba mashtaka haya yamekamilika na unaona ulibambikiziwa kesi na imechukua muda mrefu unaweza kurudi Mahakamai kufungua kesi ya madai.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza naishukuru Serikali kwa kutenga fedha na kukamilisha hilo jengo.

Je, ni kwa kiwango gani jengo hili limekuwa jumuifu kwa maana ya kuwa na Mahakama ya Mwanzo, Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mkoa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa kuna msongamano mkubwa sana katika Gereza la Ilembo pale Vwawa: Je, ni kwa kiwango gani jengo hili sasa litasaidia kuhakikisha kwamba kesi nyingi ambazo zimesongamana katika Mahakama zitaweza kwisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Naomba kujibu maswali mawili sasa ya Mheshimiwa Japhet, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza anataka kufahamu kama hili jengo litakuwa linajumuisha na Mahakama nyingine. Nimwarifu kwamba, katika mpango wetu wa Mahakama, miongoni mwa mikoa ambayo tunajenga majengo ambayo yatajumuisha Mahakama zote, ni pamoja na Mkoa wake. Kwa hiyo, hili limezingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, anataka kufahamu kama sasa kesi zitakwenda kwa kasi. Ni dhahiri kwamba kesi zitakwenda kwa kasi kwa sababu jengo hili baada ya kukamilika, efficiency ya Waheshimiwa Mahakimu wetu itaongezeka. (Makofi)
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama katika Wilaya ya Kiteto na Wilaya ya Hanang’ Mkoani Manyara?

NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Regina Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Manyara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakama yetu ina mpango wa kujenga majengo yote ya Mahakama za Wilaya na za Mwanzo katika mikoa yote Tanzania. Katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 tuna mpango wa kujenga Hanang’ pamoja na Kiteto. Kwa hiyo, Mahakama hizi ziko kwenye mpango. (Makofi)
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba nilulize swali la nyongeza. Kwamba Mahakama ya Mwanzo kule Kalya inaendelea ni kweli. Sasa nilikuwa naomba niishauri Serikali kwamba yule Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo kule Kalya basi aje kwenye Makao Makuu ya Tarafa pale Buhingu kabla jengo hilo halijajengwa la Mahakama ili aendelee kuhudumia wananchi kwa masuala ya sheria, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naomba nijibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Nashon, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kwamba Makao Makuu haya ya Mgambo na Kalya kuna umbali zaidi ya kilomita 100 na wananchi wamekuwa wakipata tabu kufikia huduma hii. Mahakama yetu ya Tanzania inaridhia maombi ya Mheshimiwa Mbunge kwamba huyo Hakimu aliyeko Kalya aende sasa Mgambo walau tumtafutie Ofisi pale kwa Afisa Tarafa ili huduma, iendelee kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge tunalipokea jambo hili na tunalifanyia kazi na huduma itatolewa. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Jiji la Arusha limetenga eneo la ekari tano kwenye Kata ya Terrat kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama mpya ya mwanzo; je ni lini Serikali itaanza ujenzi wa mahakama hii ya mwanzo kwenye Kata ya Terrat?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka huu wa fedha ambao tunashukuru Bunge lako tukufu lilitupitishia bajeti ya zaidi ya bilioni 57 fedha za nje pamoja na bilioni 31 fedha za ndani, tumepanga kujenga mahakama zaidi ya 60 na miongoni mwa maeneo ambayo tutakwenda kujenga ni eneo hili la Terrat pale Arusha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Gambo kuwa na amani mwaka huu tunajenga Mahakama katika eneo la Terrat.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je Serikali ina mpango gani wa kujenga Mahakama ya mwanzo eneo la Minjingu?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi naomba sasa kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Manyara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wetu huu wa bajeti ya mwaka huu miongoni mwa maeneo ambayo yanahitaji ujenzi wa Mahakama ni pamoja na eneo la Minjingu. Mheshimiwa Asia pamoja na wewe mmekuwa mkikumbusha jambo hili naomba niliarifu Bunge hili Tukufu na wananchi wa Babati Vijijini kwamba tutajenga Mahakama pale Minjingu ili wananchi wapate huduma.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kuwa Mahakama za Usanda na Samuye katika Halmashauri ya Shinyanga zimejengwa toka enzi ya mkoloni. Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa Mahakama hizo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru nijibu swali la Mheshimiwa Mnzava Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Shinyanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wetu wa Mahakama mwaka huu tunakwenda kujenga Mahakama zaidi ya 38 za Wilaya, Mahakama 60 za mwanzo lakini pia fedha hizi ambazo tumetenga tunakarabati pia Mahakama.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Mnzava nipokee Mahakama ambazo umezitaja tutaweka kwenye mpango wetu wa Mahakama ili tuzikarabati.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri sana na yenye matumaini kwa wananchi wa Wilaya ya Ubungo;:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa vikao vya mashauriano baina ya Wizara na Mkoa wa Dar es Salaam vinaendelea kuona uwezekano wa kujenga hiyo Sport Arena katika eneo la Luguruni la ekari 10.5 lililotolewa na Mheshimiwa Rais:-

(a) Je, Serikali au wizara mpo tayari sasa kumshirikisha Mheshimiwa Mbunge katika vikao hivyo kama mdau?

(b) Pamoja na nia nzuri ya Serikali ya kujenga Arena hiyo, ikiwa sasa tayari imeshakamilisha ile michoro yote ya Arena: Je, Serikali imeweza kuzingatia au kuweka miundombinu ya kuingia na kutoka katika Arena hizo?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mtemvu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wizara hatuna tatizo kushirikisha Wabunge. Hivyo niagize BMT na Mkurugenzi wetu wa Michezo, watakapokutana na Uongozi wa Dar es Salaam, wawashirikishe Wabunge wote wa Mkoa wa Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili alitaka kufahamu kama hiyo michoro imezingatia miundombinu mbalimbali ya kuingilia na kutokea katika viwanja hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumezingatia hili. (Makofi)
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza: Je, ni lini ujenzi wa shule 56 za michezo utaanza kama Serikali ambavyo iliahidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asia Halamga, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato umeshaanza wa kujenga Academy 56 katika shule zetu za Sekondari na tunatarajia katika mwaka huu wa fedha ambao tunauendea, endapo Bunge lako Tukufu litatupitishia fedha, tumetenga kiasi cha Shilingi bilioni mbili kwa kuanza na shule hizo.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kama ilivyo changamoto wenzangu walivyosema, sisi ma-promoter wa ngumi, wachezaji wetu wa ngumi hawana maeneo ya kufanyia mazoezi. Ni lini Serikali itajenga maeneo ya mazoezi ya mabondia wote hapa nchini Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Bondia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika viwanja hivi ambavyo nimesema tunategemea kujenga Dar es Salaam na Dodoma ambavyo viko katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi; hivi viwanja vimezingatia michezo yote, in door games pia zimezingatiwa pamoja na ngumi. (Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri ni takribani mwaka mmoja umeisha tangu Rais atoe maelekezo kwenye Wizara kufanya marekebisho ya viwanja nchini, lakini hadi sasa hakuna kiwanja kilichofanyiwa marekebisho kupitia Wizara:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ipi kauli ya Serikali kwa sababu hali ya viwanja nchini ni mbaya na bado wanamichezo wanazidi kuweka matumaini kwa Serikali?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sanga, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wizara tunashirikiana na wadau mbalimbali kurekebisha viwanja. Hivi ninavyoongea, sasa hivi tunakamilisha maridhiano na Chama cha Mapinduzi ambao wanamiliki viwanja nchi nzima kwenye mikoa, vile viwanja vikubwa, na tunategemea tutaanza ukarabati wa viwanja hivi na mwaka huu unaoanza Mheshimiwa Sanga tutaanza na viwanja saba. Tumetenga zaidi ya Shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ukarabati wa hivi viwanja. (Makofi)

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya kuendelea kuboresha mahakama zetu hapa nchini na hii itatusaidia hata ukienda kuhukumiwa kule uende vizuri vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja tu la nyongeza. Kwa kuwa Serikali ina mpango wa kujenga mahakama ikiwemo hiyo ya Urambo aliyojibu, lakini Halmashauri ya Wilaya ya Uyui mpaka leo tunatumia majengo ya Mkuu wa Wilaya: Je, ni lini Halmashauri ya Wilaya ya Uyui nayo itajengewa Mahakama ya Wilaya? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Venant Daud, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Venant Daud, Mbunge wa Uyui pamoja na Mheshimiwa Almas Maige, wamekuwa wakifatilia ujenzi wa mahakama katika Wilaya yao ya Uyui. Pia nampongeza Mheshimiwa DC kwa kutupatia ofisi yake na majengo ili kazi za mahakama ziendelee. Nimjulishe Mheshimiwa Venant kwamba tunajenga Mahakama ya Uyui mwaka huu wa fedha, na tayari utaratibu unaendelea kumpata mkandarasi.
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, hao makocha ambao amewataja, wamesoma Leseni A ya CAF mwaka 2016, mpaka leo TFF haijawapatia vyeti vyao, hali ambayo inawakwamisha kutafuta ajira nje ya nchi. Je, ni lini watapewa vyeti vyao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Ni utamaduni wa nchi yetu kulinda ajira za ndani dhidi ya wageni mpaka pale itakapothibitika taaluma hiyo haipo hapa ndani. Hapa tuna makocha wengi ambao wapo mtaani hawana kazi, lakini wageni wamekuwa wakija kwa wingi sana kufundisha vilabu vyetu hata vile vya daraja la kwanza. Wenzetu wa Zambia na Namibia wameweka utaratibu kuwalinda makocha wazawa kwa maana ya kwamba, kufundisha ligi kuu ya kwao, mpaka uwe umefundisha timu ya Taifa huko ulikotoka: Je, Serikali ya Tanzania ina mpango gani kulinda walimu wa mpira wa ndani?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Antipas Zeno, Mbunge wa Malinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, Mheshimiwa Antipas amependa kufahamu hatima ya makocha hawa ambao walipewa mafunzo mwaka 2016 chini ya TFF pamoja na CAF. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba jambo hili limekuwa likifuatiliwa kwa karibu na wenzetu wa TFF, na bahati nzuri miongoni mwa watu ambao walikuwa kwenye mafunzo haya ni pamoja na Katibu Mkuu wa TFF Kidau na jambo hili wamekuwa wakiwasiliana ni jinsi gani walimalize ili hawa makocha waweze kupata haki yao.

Swali la pili, alipenda kufahamu mkakati wa Serikali wa kuweza kuwalinda makocha wa ndani kwa sababu sasa tumeshaanza kuwazalisha. Sisi kama Wizara tunafahamu kwamba vijana wetu wanapokuwa na sifa lazima tuwalinde. Tuna mkakati wa Wizara yetu wa kukuza michezo wa mwaka 2021 mpaka 2031, miongoni mwa vitu ambavyo tunakwenda kuzingatia ni kuhakikisha tunatoa kozi kwa makocha wetu. Ndiyo maana hata sasa kozi inaendelea, zaidi ya nchi tatu zinashiriki. Watakapofuzu vijana zaidi ya 20 wa Kitanzania, maana yake wataendelea kupewa fursa, ahsante. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa niweze kuuliza swali la nyongeza. Nilipenda kufahamu: Nini mkakati wa Serikali wa kuwaandaa makocha wengi wanawake ili waweze kufanya ukocha hapa nchini na nje ya nchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati tuliyonayo pia ni kuhakikisha kwenye ile michezo yetu ya kipaumbele kwa Wizara ambayo tuna michezo sita ya kipaumbele kwa Taifa ni pamoja na kuhakikisha pia tunapata makocha wanawake. Kwa hiyo, jambo hili Mheshimiwa Toufiq tunalizingatia pia.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Tumeona michezo mbalimbali ya wanawake wanafika mbele wanaenda hadi Kombe la Dunia: Ni nini mkakati sasa wa Serikali kuhakikisha kwamba michezo yote; Volleyball, Basketball na michezo mingine tunapata makocha wanawake ambao wanaweza wakazi-train hizi timu ili ziweze kufika mbali zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Tendega, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu tumedhamiria kwa dhati kuhakikisha kwamba tunanyanyua vipaji vya wanawake wa Kitanzania. Vile vile kwenye michezo ya kipaumbele mchezo wa mpira wa miguu wanawake upo na mchezo wa mpira wa pete upo. Kazi kubwa iliyopo mbele yetu ni kuhakikisha walimu wa michezo hiyo wanatokana na wanawake wenyewe. Mheshimiwa Grace utuamini, tunaendelea na kazi hiyo.
MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza, kwa kuwa suala la michezo siyo suala la Muungano; na Zanzibar imekosa kuwa mwanachama kwa sababu ya Tanzania tayari ni mwanachama: Je, ni lini sasa TFF itabadili jina badala ya kuwa Tanzania Football Federation iwe Tanzania Bara Football Federation ili kuipa nafasi Zanzibar kuwa mwanachama? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kama hilo haliwezekani, basi ni lini Serikali itaunda MOU ili kuipa faida za kuwa mwanachama wa FIFA Zanzibar kisheria? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naomba kujibu swali la pili la Mheshimiwa Mohamed Saidi Issa, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye jibu langu la msingi nimeeleza kwamba ni kweli sisi Wizara yetu tunakiri kuna changamoto kupitia ZFF pamoja na TFF. Waziri wetu Mheshimiwa Mchengerwa ameshakutana na Mheshimiwa Waziri wa Zanzibar wa Michezo, dada yangu Mheshimiwa Tabia wamezungumza, na hivi karibuni baada ya Bunge, tutakutana na vyombo hivi viwili; ZFF pamoja na TFF ili tuweke MOU ya pamoja kuona jinsi gani Zanzibar pia inafaidika na mgao wa fedha za FIFA. (Makofi)
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Soka la Wanawake Tanzania limetuletea heshima kubwa sana. Mbali ya kwamba hatuna makocha, lakini pia hatuna waamuzi uwanjani kwenye soka la akina mama.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha tunapata waamuzi akina mama ili wasaidie katika soka hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Prof. Ndakidemi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la soka la wanawake kwetu sisi ni kipaumbele. Nawapongeza wanawake wote Tanzania kwa jinsi ambavyo wamemwelewa Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwamba tunahitaji kushiriki na kushinda. Suala la makocha pamoja na ma-referee liko kwenye mpango kazi wetu kuhakikisha kwamba tunakuwa na ma-referee pia wa kutosha.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali na hasa, sasa tunakwenda kujenga Mahakama katika Tarafa ya Bwakira Kata ya Bwakira Chini. Naipongeza Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Tarafa ya Bwakira Chini kuna hakimu ambaye anaitwa Deogratius Amatungiro, ni Hakimu ambaye amegeuza Mahakama kama duka la kuuza haki kwa wananchi kiasi ambacho wananchi wa Tarafa ya Bwakira Chini wamemchoka: Je, Mheshimiwa Waziri uko tayari kwenda nami katika Kata ya Bwakira Chini, Kata ya Kisaki na Kata ya Mngazi ambayo ndiyo Tarafa ya Bwakira, ukasikilize malalamiko ya wananchi? Kwa sababu viongozi mbalimbali wamepita lakini hakuna hatua yeyote ambayo imechukuliwa ili yeye kama msimamizi au ndiyo msimamizi katika Mahakama na Wizara ya Sheria uondoke naye huyo hakimu kwa sababu tumemchoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni lini tunatarajia kwamba hiyo Mahakama ya Bwakira Chini itaanza kujengwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru, naomba sasa nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameuliza ni lini Mahakama hii katika Kata ya Bwakara Chini itajengwa? Nilijibu katika majibu yangu ya msingi kwamba mwaka huu wa fedha mhimili wetu wa Mahakama imetenga kujenga Mahakama za Mwanzo zaidi ya 60 na tuna zaidi ya shilingi bilioni 88 ambazo Bunge hili wametupititishia. Kwa hiyo, Mheshimiwa Innocent Mahakama hii tunajenga mwaka huu na ndiyo maana nimesema Mkandarasi sasa anatafutwa ili kazi hii ianze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza, amemlalamikia Mheshimiwa Hakimu katika Mahakama hii ya Bwakira ambayo tunakwenda kujenga, japo inaendelea katika eneo la godauni. Naomba nimwelekeze Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wenzangu kwamba tuna Kamati zetu za Maadili kwa Maafisa wa Mahakama na Wenyeviti wa Kamati hizi ni Ma-DC wetu katika Wilaya zetu lakini na Waheshimiwa Ma-RC. Kwa hiyo, Mheshimiwa Innocent kwa kuwa kanuni zetu zinatuhitaji, kama kuna malalamiko yoyote kwa Maafisa wetu wa Mahakama, tunapaswa kuandika kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge aandike kwa maandishi ampelekee Mheshimiwa DC wa Morogoro ili Kamati ya Maadili ya Maafisa wa Mahakama katika Wilaya yake sasa waanze uchunguzi, na kama kuna tuhuma zitakuwa zimethibitika, basi hatua zitachukuliwa, ahsante.