Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Pauline Philipo Gekul (4 total)

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nimuulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, hivi karibuni Serikali imetoa Waraka katika Halmashauri zetu kuhusu elimu bure na Waraka wenyewe ni wa tarehe 6 Januari, 2016.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, Waraka huu umezua sintofahamu katika sehemu ya chakula cha wanafunzi katika shule zetu. Mfano, Waraka huu unasema kwamba wanafunzi wanaosoma day wazazi walipe chakula, lakini wanafunzi wanaosoma shule za bweni ambao wazazi wao wana uwezo hata wameweza kuwafikisha katika shule hizo, hawatakiwi kulipa hata chakula, Serikali itapeleka chakula.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali inasemaje katika hali hii ambayo imezua mtafaruku kwa wazazi kuona kwamba wamebaguliwa wale ambao hawana uwezo na Serikali imewaongezea uwezo wale ambao kidogo wana uwezo?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Philip Gekul, Mbunge wa Jimbo la Babati Mjini kama ifuatavyo:-
Ni kweli kwamba ipo mikanganyiko imejitokeza sana hasa baada ya kuwa tumeanza kutekeleza mfumo wa elimu bure. Hata hivyo, nataka niwajulishe Watanzania wote maeneo ambayo Serikali imejikita, kuwa ni ya bure.
Moja, kwa upande wa sekondari, tulikuwa na ada ya shilingi 20,000/= kwa mwaka kwa shule za kutwa, eneo hilo sasa hawatalipa. Eneo la sekondari za bweni, wazazi walikuwa wanalipa shilingi 70,000/= kwa mwaka eneo hilo halilipiwi, ni bure. Eneo la tatu, kwa shule za msingi na sekondari mitihani yote ya darasa la nne na kidato cha pili, iliyokuwa inafanywa kwa wanafunzi kuchangia, eneo hilo sasa wanafunzi hawatachangia. Serikali itatenga fedha kwa ajili ya mitihani hiyo ya kidato cha pili na darasa la nne, watafanya bure.
Mheshimiwa Spika, eneo la lingine kwa shule za sekondari za bweni ambazo wanakula chakula tunaendelea na utaratibu wa kuwalipia, kuwagharamia. Sasa mkanganyiko unaojitokeza kwa uelewa wangu, Mheshimiwa Mbunge na Watanzania wote, ni pale ambako zipo shule za kutwa, ambazo kisera shule za kutwa, ni za mtoto anatoka nyumbani anaenda shuleni, anasoma anarudi kula nyumbani. Hizi sasa ndiyo ambazo zimeleta mkanganyiko hasa kwa wazazi ambao walikuwa wamejiwekea mpango wao, wao wenyewe ili kuweza kuwafanya vijana wetu waweze kupata lishe shuleni.
Mheshimiwa Spika, katika eneo hili nikiri kwamba pamoja na mkanganyiko ikiwemo na hili, Wizara sasa inaandaa utaratibu mzuri wa maelezo mazuri ya namna tutakavyotekeleza kwenye eneo hili halafu tutatoa taarifa, kwa sababu ndiyo tumeanza kutekeleza mwezi Januari, hizi changamoto zimeanza kujitokeza, yako maeneo mengine wanaendelea kuchangisha. Kwa hiyo, tunataka tutoe Waraka ambao sasa utaweka wazi kila kitu na Waheshimiwa Wabunge, tutawaletea nakala ili mtusaidie katika kuratibu jambo hili. (Makofi)
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imekuwa ikitoa kauli na matamko mbalimbali kwa wakulima wa mbaazi kote nchini kwamba Serikali inafanya mazungumzo na Serikali ya India ili wakulima hawa wapatiwe soko. Hata hivyo hadi sasa mazungumzo hayo hayajakamilika na wakulima wamebaki na mazao yao.

Mheshimiwa Spika, ninaomba nifahamu, kwa nini Serikali isione ni busara kuwatangazia wakulima wa mbaazi kote nchini kwamba wameshindwa kuwapatia soko na wasiende kulima katika msimu huu wa kilimo ambao unakwenda kuanza sasa?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gekul, Mbunge wa Babati Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hata juzi wakati tunapeana maelekezo ya msingi jambo hili la matatizo ya masoko ya mazao yetu lilijitokeza, mbaazi ikiwemo. Ninachoweza kusema hatuwezi kuwaambia wakulima msimu huu wasijiandae kulima kwa sababu suala la masoko, awali zao la mbaazi tulikuwa na soko la uhakika la nchi ya India na ndio wanunuzi wakuu wa zao hili. Huku kwetu sisi mikoa yote inayolima imeendelea kulima kila mwaka na tumeendelea kufanya biashara na nchi ya India bila tatizo lolote lile.

Mheshimiwa Spika, lakini pia hata hivi karibuni Waziri Mkuu wa India alipokuja nchini, aliweza kusisitiza pia tulime mbaazi nyingi na wao pia wanalima na sisi tumelima. Sasa tulipofikia hatua ya kuuza kwa bahati mbaya au nzuri kwao nchi ya India imeweza kuzalisha mbaazi kwa asilimia 30 zaidi na kwa maana hiyo wana mbaazi ziada na kwa hiyo, walisitisha utaratibu wa kununua mbaazi kutoka nchi za nje kuingiza kwao mpaka hapo akiba yao watakapoifikiria vinginevyo. Kwa kufanya hilo wametuathiri kwa sababu soko pekee la mbaazi kwetu sisi ilikuwa ni nchi ya India.

Mheshimiwa Spika, sasa nini jukumu la Serikali kwa sasa; tunaendelea kutafuta masoko na ndiyo sababu tumewasihi wakulima wa mbaazi nchini kote, na ni mikoa mingi inayolima sana mbaazi, tumeendelea kuwasihi kwamba waendelee kutusubiri kwa sababu Bodi ya Mazao Mchanganyiko ambayo inashughulikia mbaazi pia sasa inaendelea kutafuta masoko, likiwemo na lile zao la tumbaku ambalo nimelieleza muda mfupi uliopita.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jitihada hizi zitakapofikia hatua nzuri, tutauza. Kwa sasa hatuwezi kuwaambia kwamba tutauza kwa sababu bado negotiations zinaendelea na mataifa ambayo yatataka kununua zao hili la mbaazi ikiwemo na India yenyewe kwa sababu ya ile commitment ambayo ilikuwa imeshatolewa kati yetu na wao; na ndiyo utaratibu wa kawaida kwa nchi ambazo tunafanya nao biashara za mazao. Pale ambapo kunatokea tatizo lazima na sisi tupate taarifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hii ni taarifa kwa wakulima wote wa mbaazi kwamba kwa sasa wawe watulivu, tunaendelea na utaratibu huu wakati wowote tutawapa taarifa. Ni kweli tunajua wanaathirika sana lakini ni muhimu pia taarifa hii kuwa nayo na uvumilivu ni muhimu pia kuwa nao.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kunipa nafasi nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu swali. Ni sera na ni azma ya Serikali yetu kuwapatia wananchi maji salama lakini kwa bei nafuu pia kwa sababu maji ni huduma si biashara. Niipongeze Serikali yetu kwa kufikia azma hiyo hiyo mijini kwa zaidi ya asilimia 80 na vijijini kwa asilimia 70.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana EWURA walipandisha bili za maji kote nchini, jambo ambali limesababisha wananchi wengi kushindwa kulipa bili hizo. Serikali pamoja na wewe Mheshimiwa Waziri Mkuu mlituahidi hapa Bungeni kwamba EWURA wacheki upya mchakato wao ili waona kama hizi bili zinaweza zikashuka ili wananchi waweze kulipia. Naomba nifahamu Mheshimiwa Waziri Mkuu ni lini mchakato wa EWURA utakamilika ili hizi bili zishuke kwa sababu wananchi wengi wameshindwa kulipia; mfano wananchi wa Babati Mjini? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gekul Mbunge wa Babati Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nimewahi kupokea malalamiko haya kutoka hapa Bungeni, kutoka kwenye mikutano ninayoifanya kwenye maeneo mbalimbali nchini juu ya upandaji wa bei za maji holela na kukwaza wananchi kumudu kupata huduma hiyo ya maji. Kwanza nataka niwahakikishie Watanzania kwamba Serikali yetu imejipanga kutoa huduma za maji mpka kuingia vijijini kama ambavyo tumeeleza na kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameeleza. Kwamba tunahitaji sasa angalau kila kijiji kiwe na angalau kiwekwe kisima kama ni kifupi tupate maji ili wananchi wawe na uhakika wapi watapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hiyo inaendelea vizuri na Wizara yetu ya maji inasimamia kuhakikisha kwamba huduma za maji zinapatikana kwa ujenzi wa miradi ya visima vifupi, vya kati lakini pia hata miradi mikubwa ambayo wakati wote tumekuwa tukiieleza. Maji haya Serikali hailengi kufanya biashara kwa wananchi wala hatuhitaji faida kutoka kwa wananchi, muhimu wa utoaji huduma ya maji kwa wananchi ni kufikisha maji kwa wananchi wayapate maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeunda Kamati zinazosimamia maji kwenye maeneo husika; na pia tumeunda mamlaka ya jumla ambayo inasimamia utoaji wa huduma ya maji kwenye ngazi ya Wilaya RUWASA; kwenye ngazi ya Kitaifa tuna zile mamlaka ambazo zinachukua unaweza ukawa ni Mikoa miwili au mitatu au Kanda kusimamia utoaji huduma lakini pia na ujenzi wa miradi mipya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati hizi tumezitaka zifanye mapitio ya huduma ndogondogo zinazohitaji kwa ajili ya ukarabati wa kuendesha mradi huo kwenye maeneo yao; kama vile kununua tap na kufanya mabadiliko ya bomba lililotoboka. Hiyo tumeiachia zile Kamati ziratibu na sasa Kamati hizi zinahitaji angalau wananchi wachangia huduma ya maji kwenye eneo lao. Huduma hii hatutarajii kusikia mwananchi analipa gharama kubwa inayomshinda na lile ndilo tuliloagiza kwa Wizara. Tumeweka utaratibu EWURA wafanye mapitio ya maeneo haya kuona kwamba gharama haziwi zaidi ya mapato ya mwananchi kwenye eneo lake ili kuongoa usumbufu au dhana ya kwamba tunatoa huduma ya maji kama vile biashara, hapana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumeweka utaratibu EWURA wafanye mapitio ya maeneo haya kuona kwamba, gharama haziwi zaidi ya mapato ya mwananchi kwenye eneo lake, ili kuondoa usumbufu au dhana ya kwamba, tunatoa huduma ya maji kama vile biashara, hapana. Agizo limeshatolewa na Wizara ya Maji imeshatekeleza. kwa hiyo nitamuagiza Waziri wa Maji atupe taarifa ya hatua waliyoifikia ili sasa tuone kuwa huduma hii inatolewa huko kwa namna ambazo mwananchi anaweza kupata maji akaendelea kuhudumiwa. Vilevile kama kijiji, kata, waendelee kufanya ukarabati mdogomdogo ili kufanya mradi huo kuendelea kutoa huduma kwa wananchi wake. Asante sana. (Makofi)
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa niulize swali kwa Waziri Mkuu, ni azma ya Serikali yetu na ni Sera ya Serikali yetu kuwapatia wananchi maji safi na salama lakini kwa bei nafuu. Nafahamu pia mchakato wa Serikali kupandisha bili za maji kupitia mamlaka za maji kufanya public hearing na mwisho EWURA waweze kufanya maamuzi ya bili hizo.

Mheshimiwa Spika, EWURA wamemaliza mchakato bahati mbaya sana maoni ya wananchi hayajazingatiwa, bili hizi za maji kote nchini zimepanda kwa zaidi ya asilimia 80. Mfano, mtumiaji wa maji nyumbani alikuwa analipa unit 1 kwa shilingi 1,195 imepanda kuanzia hapo mpaka 1,800. Naomba nifahamu kauli ya Serikali juu ya ongezeko hili la zaidi ya asilimia 80 ya bili za maji nchini wakati wananchi waliomba kwamba bili hizi zisipande?(Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gekul, Mbunge wa Babati Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, azma ya Serikali katika kutoa huduma mbalimbali nchini bado ni njema na inawaangalia uwezo wa Watanzania mpaka yule mwananchi wa chini wanaweza kumudu kugharamia gharama hizo kwa uwezo wake wa kifedha. Umeeleza upo mchakato unaendelea na umeishia mahali ambapo gharama zimepanda kwa asilimia 80. Sisi Serikali tumetoa mamlaka kwenye hizi wakala ili kufanya mapitio na mapitio hayo lazima yaangalie uwezo wa wananchi wenyewe nchini ili wawezeshe wananchi kupata huduma hiyo kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nimepata taarifa kwamba EWURA na Wizara ya Maji kupitia wakala wamekaa vikao vyao na sasa wameshatoa taarifa ya mwisho ya gharama hizo na zimefikia kwa kiwango ulichokitaja ambacho kimepanda kwa asilimia 80 lakini utaratibu Serikalini ni kwamba baada ya kuwa maazimio hayo yamefanywa, wanatoa taarifa Serikalini. Nashukuru kwamba umetuambia hilo na tumepata taarifa kwamba hata wadau hawakuweza kupata fursa ya kusikilizwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni jukumu la Serikali sasa baada ya kupata matokeo yale, baada ya wao mjadala wao wataleta Serikalini tuone kwamba je, viwango walivyotoa vinawezesha Watanzania kupata huduma hiyo? Na tutakapogundua kwamba hawawezeshwi kupata huduma hiyo, basi Serikali itafanya maamuzi mengine dhidi ya hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikutake ufanye subira, EWURA walete matokeo ya vikao vyao na mapendekezo yao, Serikali tutafanya maamuzi kwa kushirikiana na Wizara ya Maji. Tukishawapa taarifa hiyo ya mwisho ndiyo itakuwa ndiyo bei ambazo zitakuwa zinatumika na mamlaka hiyo, ahsante. (Makofi)