Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Additional Questions to the Prime Minister from Hon. Hassan Elias Masala (1 total)

MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, kupitia Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ambayo imenadiwa na Mheshimiwa John Pombe Magufuli mwaka 2015; moja ya ahadi kubwa ambayo ilitolewa kwa Watanzania ni ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami. Naomba kufahamu kupitia Serikali yetu, imejipanga vipi katika kutekeleza ahadi hii ambayo kimsingi inasubiriwa na Watanzania walio wengi?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Masala, Mbunge wa Jimbo la Nachingwea, Mkoani Lindi, kama ifuatavyo:-
Kwanza, nataka niwaambie Watanzania kwamba Chama cha Mapinduzi kupitia Ilani yake ya Uchaguzi ya mwaka 2015 imefafanua mambo mengi ambayo tumeamua tuyatekeleze katika kipindi cha miaka mitano. Jambo ambalo Mheshimiwa Mbunge ametaka kujua utekelezaji wake ni lini, nataka nimhakikishie kwamba ahadi zetu zote zilizoahidiwa na Chama cha Mapinduzi zitatekelezwa kama ambavyo zimeahidiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumedhamiria kujenga barabara zetu kwa kiwango cha lami na tumeanza na mkakati wa kuunganisha barabara za ngazi za Mikoa, zinazounganisha Mikoa kwa Mikoa; tukishakamilisha hizo, tunaingia kwenye barabara zinazounganisha ngazi za Wilaya na barabara zote ambazo zimeainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa awamu hii ni barabara ambazo zitakamilishwa kupitia bajeti ambayo sasa mnaipitisha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ujenzi itakapokuja hapa, naomba niwashawishi Waheshimiwa Wabunge kuweza kuipitisha ili tuanze kazi ya kukamilisha barabara ambazo nimezitaja. Pale ambapo barabara za Mikoa hazijakamilika, tunataka tuzikamilishe. Tukishakamilisha hizo zote, tunaanza ngazi za Wilaya ili tuendelee.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka niwahakikishie Watanzania wote kwamba ahadi zote zilizotolewa na Mheshimiwa Rais kwa kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 zitakamilishwa kama zilivyoahidiwa. Ahsante sana.