Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Juliana Daniel Shonza (18 total)

MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza:-
Tatizo la maji ni changamoto kubwa sana katika Mkoa wa Songwe na Wilaya zake zote:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaondolea adha ya maji wanawake wa Mkoa huu hususan Mji Mdogo wa Tunduma ambako hali ni tete zaidi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua adha kubwa ya tatizo la maji inayowakabili wananchi wa Mkoa wa Songwe hususan wanawake. Katika mpango wa muda mrefu wa uboreshaji wa huduma ya majisafi Mkoa wa Songwe, Serikali imekamilisha usanifu na uandaaji wa vitabu vya zabuni kwa ajili ya kuboresha huduma ya majisafi katika Miji ya Mkoa wa Songwe ikiwemo Vwawa ambako ni Makao Makuu ya Mkoa, Itumba, Isongole pamoja na Tunduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha za kutekeleza mradi huo kutoka kwa wafadhili mbalimbali. Kwa sasa Serikali imewasilisha maombi katika Benki ya Maendeleo ya Ufaransa ya kupata mkopo wa masharti nafuu kwa ajili ya kutekeleza mradi wa majisafi Mjini Tunduma. Pia Serikali imewasilisha maandiko ya miradi ya majisafi kwa Miji ya Vwawa na Tunduma kwenda Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) kwa ajili ya kutafuta fedha za kutekeleza miradi hiyo Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika mpango wa muda mfupi wa kuboresha huduma ya maji kwa Miji ya Vwawa na Tunduma, Serikali katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya upanuzi wa mfumo wa usambazaji wa maji katika miji hiyo.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza:-
Benki nyingi nchini zimekuwa na Riba kubwa, hali ambayo inafanya wanawake washindwe kukopa kujiinua kiuchumi. Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka Benki ya Wanawake Mkoa wa Songwe ili wanawake wajasiriamali wanufaike na mikopo hii ya riba nafuu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Benki ya Wanawake Tanzania ni kusambaza huduma zake katika maeneo yote ya Tanzania ikiwemo Mkoa wa Songwe. Hata hivyo, azma hii inakwamishwa na mtaji mdogo wa benki hii, ndiyo maana kwa sasa imejikita zaidi katika kutoa huduma zake kwa kutumia vituo vya mikopo ambapo hadi sasa benki ina vituo 89 katika mikoa saba ukiwemo Mkoa wa Mbeya ambao hadi mwaka 2015 ulikuwa sehemu ya Mkoa huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango mkakati wa Benki ya Wanawake wa mwaka 2014/2017 ni kufungua angalau matawi matatu kila mwaka. Hii itawezekana tu endapo mtaji wa benki utakuwa kama inavyotegemewa. Hivyo benki itauingiza Mkoa mpya wa Songwe kwenye mipango yake ya upanuzi wa huduma kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JULIANA D. SHONZA Aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha miundombinu ya elimu vijijini kama nyumba za walimu pamoja na kulipa malimbikizo ya madeni ya walimu wanayoidai Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inaboresha miundombinu ya shule nchini kupitia mipango na bajeti ya Serikali kwa kushirikisha nguvu za wananchi na wadau wa maendeleo ili kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia.
Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imetenga shilingi bilioni 13.9 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu 1,157 kwa shule za msingi na shilingi bilioni 11.14 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu 661 kwa shule za sekondari. Aidha, kupitia Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES II), Serikali imekamilisha ujenzi wa nyumba 146 kati ya nyumba 183 ambazo kila nyumba wataishi watumishi sita (walimu). Ujenzi wa nyumba hizo umegharimu shilingi bilioni 21.9. Nyumba 37 zinaendelea kujengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 5.5 na zitakamilika tarehe 30 Aprili, 2017.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kulipa madeni ya walimu kadri yanavyojitokeza na kuhakikiwa. Katika mwezi Oktoba, 2015 Serikali ililipa madeni ya shilingi bilioni 20.12 kwa walimu 44,700 na shilingi bilioni 1.107 zililipwa mwezi Februari, 2016 kwa walimu 3,221. Hivi sasa walimu wanadai Serikali madeni yanayofikia shilingi bilioni 26.04 kwa ajili ya walimu waliopo kazini 33,620 na walimu wastaafu 2,134. Deni hilo limewasilishwa Hazina kwa ajili ya taratibu za mwisho za kulipwa kwa walimu wanaodai.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza:-
Hospitali ya Vwawa Wilayani Mbozi inakabiliwa na changamoto kubwa ya uhaba wa vitanda vya kulalia wajawazito pamoja na vile vya kujifungulia, pia wodi ya akinamama ni ndogo huku ukizingatia kuwa hospitali hiyo inahudumia Wilaya ya Mbozi na Momba:-
Je, ni lini Serikali itajenga wodi ya akinamama kubwa yenye vifaa vya kutosha ili wanawake hawa waondokane na adha ya kulala wawili wawili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Wilaya ya Mbozi yaani Vwawa ni hospitali iliyopandishwa hadhi kutoka Kituo cha Afya kuanzia mwaka 2001. Kwa sasa hospitali hiyo inahudumia wagonjwa wengi kutoka Halmashauri ya Mji wa Tunduma, Wilaya za Momba, Mbozi na Ileje. Ili kuboresha huduma ya uzazi katika hospitali hiyo, Serikali katika mwaka wa fedha 2017/2018, imepanga kutumia jumla ya shilingi milioni 180 kwa ajili ya ukarabati wa wodi ya wazazi baada ya kujifungua (post natal ward) ambayo itakuwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa wengi kwa wakati mmoja na kuondoa msongamano uliopo hivi sasa.
MHE. JULIANA D. SHOZA aliuliza:-
Mkoa wa Songwe ni mpya na unakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa Vyuo Vikuu hata vile vya Ufundi.
Je, ni lini Serikali itakuja na mpango wa kujenga hata kampasi ya Chuo Kikuu kimojawapo pamoja na vile Vyuo vya Ufundi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) hivi karibuni itaanza kutoa mafunzo katika kampasi yake ya Myunga iliyopo Wilaya ya Momba, Mkoa wa Songwe. Vilevile kutokana na gharama kubwa ya uwekezaji inayohitajika katika kuanzisha Vyuo Vikuu pamoja na Vyuo vya Ufundi Stadi, wananchi wanashauriwa kuendelea kutumia Vyuo Vikuu na Vyuo vya Ufundi Stadi vilivyopo nchini.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji 127 vilivyobaki vya Mkoa wa Songwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Songwe una jumla ya vijiji 307 ambapo kati ya hivyo, vijiji 180 tayari vimeapatiwa umeme na vijiji 127 bado havijapatiwa umeme. Nia ya Serikali ni kuvipatia umeme vijiji vyote visivyo na umeme kabla ya mwisho wa mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme katika vijiji vyote ambavyo havijafikiwa na umeme Tanzania Bara. Vijiji 127 vilivyobaki katika Mkoa wa Songwe vitapatiwa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ambapo utekelezaji wake ulianza mwezi Machi, 2021 na unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, kazi za mradi kwa Mkoa wa Songwe zinajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 1,065.4, msongo wa kilovoti 0.4 urefu wa kilomita 120, ufungaji wa transfoma 120 za 50kVA, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 2,640. Gharama ya mradi huu ni takriban shilingi bilioni 38.7.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE K.n.y. MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje kutatua changamoto ya msongamano wa magari yanayovuka kuelekea nchi jirani kupitia mpaka wa Tunduma?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kukabiliana na changamoto ya msongamano wa magari katika Kituo cha Forodha Tunduma. Hatua hizo ni pamoja na kutekeleza mpango wa kurasimisha utaratibu wa kubadilishana taarifa za mizigo kati ya Dar es Salaam na Nakonde, Zambia; kuendelea kutoa huduma za forodha kwa muda wa saa 24; kuimarisha mifumo ya TEHAMA ya pande mbili ili kuwezesha taarifa za mizigo inayotoka katika Bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia kusomana kwa wakati; na kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa makubaliano baina ya pande mbili ya Januari, 2020 kuhusu mkakati wa kuboresha miundombinu ya barabara pamoja na ujenzi wa maeneo ya maegesho ya magari kwa upande wa Zambia.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Zambia zitaendelea kuimarisha utendaji wa taasisi zote zinazohusika na shughuli za forodha katika Kituo cha Tunduma, pamoja na kuboresha mifumo ya TEHAMA na miundombinu ya barabara ili kukabiliana na changamoto ya msongamano wa magari.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, ni lini jengo jipya la hospitali lililojengwa Tunduma litafunguliwa na kuanza kutoa huduma kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuboresha huduma za afya nchini kwa kutoa fedha za ukarabati na ujenzi wa vituo vya kutolea huduma za afya. Serikali imeupatia Mkoa wa Songwe kiasi cha shilingi billion 14.8 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali nne kwenye Halmashauri ya Mji wa Tunduma, Halmashauri ya Wilaya ya Songwe, Momba na Ileje.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeeendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji Tunduma ambao mpaka kukamilika inakadiriwa kugharimu shilingi bilioni 9.5. Mradi huu unatekelezwa kwa awamu mbili, ambapo awamu ya kwanza utahusisha ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD) uliogharimu kiasi cha shilingi bilioni nne. Ujenzi wa jengo hilo la ghorofa moja upo kwenye hatua ya umaliziaji. Kuanzia Julai 2021 jengo hilo lilianza kutumika kutoa huduma ya wagonjwa wa nje na kliniki ya mama wajawazito na watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Tunduma. Ujenzio huo wa majengo yatakayohusishwa ni pamoja na jengo la maabara, jengo la mionzi, jengo la huduma za dharura, jengo la afya ya kinywa na meno, macho, upasuaji na utawala.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga wodi mpya ya akinamama Wilayani Mbozi itakayokuwa na nafasi ya kutosha kwa ajili ya akinamama wengi kujifungua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali Mpya ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe itakayogharimu jumla ya shilingi bilioni 12.26 mpaka kukamilika kwake. Hadi kufikia Disemba 2021 shilingi bilioni 9.8 imetolewa, ambapo jengo la OPD limekamilika na ujenzi wa wodi ya mama na mtoto unaendelea na unatarajiwa kukamilika Disemba, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga Shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Mbozi ambayo kwa sasa inatumika kama Hospitali Teule ya Mkoa wa Songwe.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, nini mkakati wa Serikali kujenga chumba cha upasuaji kwa ajili ya Wajawazito katika Kituo cha Afya cha Itaka Wilayani Mbozi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imepeleka shilingi milioni 300 kwenye Kituo cha Afya Itaka katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi. Fedha hizo zinatumika kujenga jengo la wazazi, na jengo la upasuaji. Ujenzi wa majengo hayo upo katika hatua ya msingi.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, hadi sasa mpango wa kutatua kero ya maji katika Mji wa Tunduma umefikia hatua gani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, lengo la Serikali ni kuhakikisha huduma ya upatikanaji ya maji safi na salama inaboreshwa katika Mji wa Tunduma na maeneo yote hapa nchini. Katika Mji wa Tunduma, Serikali inaendelea na upanuzi wa mtandao wa usambazaji maji kilometa10.5 ambapo Kata ya Uwanjani, Tunduma na Makambini zitaanza kupata huduma mwezi Machi, 2023.

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2022/2023, Serikali imedhamiria kutekeleza mradi wa kutumia Chanzo cha Mto Bupigi kilichopo katika Wilaya ya Ileje na taratibu za kumpata Mkandarasi zinaendelea na ujenzi wa mradi utaanza kabla ya mwezi Julai, 2023. Mradi huu umepangwa kuhudumia Miji ya Tunduma, Vwawa Mlowo, vijiji 14 vya Ileje na maeneo ambayo bomba kuu litapita. (Makofi)
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka Watumishi wa Afya wa kutosha katika Kituo cha Afya cha Itaka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuajiri na kuwapeleka watumishi katika vituo vya kutolea huduma za afya kote nchini ambapo katika ajira za mwaka 2020/2021 Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi ilipelekewa watumishi 17 na kati yao watumishi Wawili walipelekwa Kituo cha Afya Itaka.

Mheshimiwa Spika, katika ajira za watumishi wa kada za afya 7,612 zilizotangazwa wiki hii, Kituo cha Afya Itaka kitapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, lini ujenzi wa kivuko cha waenda kwa miguu katika eneo la Kisimani barabara kuu itokayo Custom kwenda Sumbawanga itaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika eneo la Kisimani lililoko kwenye Barabara ya Tunduma kwenda Sumbawanga, kumewekwa alama za kuvuka (Pundamilia – Zebra Crossings) na Taa za kuongoza magari na watembea kwa miguu zimewekwa sehemu mbili; ya kwanza mita 300 kutoka eneo la Kisimani na ya pili mita 500 kutoka taa za kwanza za kuongozea magari na watembea kwa miguu (Traffic Signals). Aidha, Serikali ina mpango wa kujenga kivuko cha chini (underpass) katika eneo la Kisimani na utekelezaji wake unategemea upatikanaji wa fedha ahsante.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE K.n.y. MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, lini Serikali itatekeleza ahadi ya ujenzi wa barabara ya Km 10 kwa kiwango cha lami Mjini Tunduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli mwaka 2020 Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliahidi ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami yenye urefu wa kilometa 10 kwenye Mji wa Tunduma.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa ahadi hiyo umeanza ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022 jumla ya kilometa 2.8 zilijengwa kwa kiwango cha lami na shilingi bilioni 1.39 zilitumika. Aidha, mwaka wa fedha wa 2022/2023 shilingi bilioni 2.3 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa kilomita 3.7 kwa kiwango cha lami ambapo shilingi bilioni 1.64 zimepokelewa na ujenzi umefikia asilimia 45.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kukamilisha ahadi hiyo kadiri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, lini ahadi ya kupeleka mradi mkubwa wa maji Tunduma utatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua tatizo la maji linaloukabili Mji wa Tunduma na hatua mbalimbali zinaendelea kuchukuliwa. Katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali inakarabati miradi ya Uhuru, Nyerere, Ipito, Tunduma na miundombinu ya maji safi Mjini Tunduma. Ukarabati huo unatarajiwa kukamilika mwezi Disemba, 2023 na kunufaisha wakazi 37,853 katika Mji wa Tunduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2023/2024, Serikali itaanza kutekeleza mradi mkubwa wa maji kupitia chanzo cha Mto Momba na kwa sasa taratibu za kuajiri Mkandarasi zinaendelea. Kukamilika kwa mradi huo kutaondoa tatizo la upatikanaji wa huduma ya maji katika Mji huo.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE K.n.y. MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, ni lini changamoto ya upatikanaji maji Mji wa Mlowo itatatuliwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua adha ya maji wanayoipata wakazi wa Mji wa Mlowo ambapo hali ya upatikanaji wa huduma hiyo ni asilimia 49. Katika kukabiliana na hali hiyo, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali inatekeleza miradi mitatu ambayo ni Mradi wa Uboreshaji Huduma ya Maji Mlowo ambao umekamilika mwezi April 2023, na inaendelea na utekelezaji wa Mradi wa Upanuzi wa Mtandao wa maji Vwawa-Mlowo na Mradi wa Ukarabati wa Chanzo cha Maji Mwansyana na Mlowo. Miradi hii inatarajia kukamilika mwezi Septemba, 2023 na kuongeza hali ya upatikanaji wa huduma ya maji Mlowo kufikia asilimia 65.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Serikali imepanga kujenga miradi mingine miwili ambayo ni Mradi wa Maji kupitia chanzo cha Mto Mafumbo, na Mradi wa Maji wa Vwawa-Mlowo na Tunduma kupitia chanzo cha Mto Momba. Miradi hiyo ipo kwenye hatua ya manunuzi ya Wakandarasi na ujenzi utaanza katika mwaka wa fedha 2023/2024 na kutekelezwa kwa kipindi cha miaka miwili. Kukamilika kwa miradi hiyo kutawezesha wakazi wa Mji Mlowo kupata huduma ya majisafi, salama na yenye kutosheleza.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwatua ndoo kichwani wanawake wa Mji wa Mlowo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ni kuhakikisha huduma ya upatikanaji wa maji inaboreshwa nchi nzima. Hali ya upatikanaji wa maji katika Mji wa Mlowo ni wastani wa asilimia 44.5. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imekamilisha mradi wa maji wa Selewa - Mlowo ambapo mradi wa maji wa Mahenje - Mlowo utakamilika mwezi Juni, 2022. Miradi hii itaboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa asilimia 53.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali itatekeleza mradi kwa kutumia chanzo cha maji cha Mto Bupigu ulioko Wilayani Ileje. Aidha, mpango wa muda mrefu ni kujenga miundombinu ya kuchukua maji kutoka mradi mkubwa wa Mto Kiwira ambao utahudumia Jiji la Mbeya na maeneo jirani ikiwemo Mji wa Mlowo na maeneo ya pembezoni.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE K.n.y MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kituo cha Polisi Mji Mdogo wa Mlowo baada ya kilichopo kuwekewa alama ya kubomolewa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali itaanza ujenzi wa kituo cha Polisi Mji Mdogo wa Mlowo baada ya Halmashauri kuzingatia na kutekeleza maagizo ya Kamati ya Usalama ya Mkoa ambayo ni kupata eneo la kutosha, kujenga kituo na nyumba za Askari, Wakaguzi na Maofisa na kuandaa Hati Miliki ya eneo litakalopatikana.