Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Hamidu Hassan Bobali (1 total)

MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kumuuliza swali moja Mheshimiwa Waziri Mkuu linalofanana kidogo na swali alilouliza Mheshimiwa Kuchauka.

Mheshimiwa Spika, wiki mbili zilizopita Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuwa Mkoani Mtwara na akatoa maagizo kwa timu zote zinazofanya uhakiki wa kupitia mashamba ya wakulima ziwe zimekamilisha zoezi lile ifikapo tarahe 5 Februari, 2019. Leo tunapongea tarahe 7 Februari, 2019 wakulima wengi wenye korosho zinazoanzia tani moja na nusu na kuendelea bado hawajafikiwa na zoezi hili la uhakiki.

Mheshimiwa Spika, nataka kupata majibu ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba kwa kuwa mpaka leo bado watu hawajafikiwa na uhakiki, nini kauli ya Serikali kwamba inaongeza siku za uhakiki au kwamba zoezi ndiyo limefikia mwisho ili wakulima waweze kujua kwa sababu hawaoni hizo timu za uhakiki zikiwaendea kwenda kuwahakiki? Nakushukuru sana.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Bobali, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mchakato wa uuzaji wa zao hili la korosho kulikuwa na eneo ilikuwa ni lazima tufanye uhakiki hasa wale wenye korosho zaidi ya kilo 1,500 na ili kuwatambua ilikuwa ni lazima tujiridhishe kama korosho ni zake kwa kufanya uhakiki? Awali utaratibu huu ulikuwa unafanywa na Bodi ya Mazao Mchanganyiko pekee jambo ambalo lilihusisha watumishi wengi lakini bado walikuwa hawakidhi mahitaji ya ukubwa wa maeneo ya wakulima wa korosho.

Mheshimiwa Spika, baada ya kugundua kwamba kulikuwa na tatizo hilo, nilipokuwa Mkoani Mtwara nilitoa maelekezo mapya na nilikuwa na tarehe 27 na ndipo nilitoa maagizo kwamba utaratibu wa uhakiki ushuke chini uhusishe Mamlaka za Serikali za Mitaa, kwa maana ya Halmashauri ambako pia tunajua tuna Mkuu wa Wilaya mwenye Kamati ya Ulinzi na Usalama lakini tuna Mkurugenzi ana Afisa Ushirika na Maafisa Kilimo waunde timu zifanye kazi ya uhakiki baada ya kuwa wamepewa majina ya watu wao wenye kilo zaidi ya 1,500 kwenye maeneo yao. Hizi wilaya zina utofauti wa ukubwa na idadi ya wakulima, kwa hiyo kuanzia tarehe 28 kama walikuwa wameshaanza kujipanga mpaka tarehe 5, inaweza kuwa baadhi ya wilaya ambazo ni kubwa sana kama ambavyo unasema Mheshimiwa hawajakamilisha lakini zoezi hilo halikomi na kuwaacha ambao hawajahakikiwa kuwa wasihakikiwe. Tarehe ile ilikuwa ni ya kimkakati wahakikishe wanafanya kwa haraka, wanawafikia wakulima ili kila mmoja awe ameshahakikiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini uzuri ni kwamba wilaya kadhaa ambazo zina idadi ndogo ya wakulima waliolima korosho na kufikia kilo 1,500 zoezi limekamilika na sasa wanasubiri ulipwaji. Wilaya zile kubwa kama Tandahimba, Nanyamba, Newala, Masasi, Nanyumbu, Liwale, Nachingwea karibu wilaya nyingi, kama vile Rufiji, ni wilaya kubwa na kama Bodi ile ilikuwa na idadi ndogo ya watu wa uhakiki kuna uwezekano wakaongeza. Sisi tunasema muhimu zaidi wakulima wahakikiwe kila mmoja aweze kupata haki yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupitia kwako nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kila mkulima atahakikiwa lakini naamini mpaka tarehe 5 idadi kubwa kwa sababu ya msisitizo watakuwa wameshafikiwa na wote watalipwa. Kwa hiyo, wale wote ambao hawajafikiwa watafikiwa na watafanyiwa uhakiki kwa haraka zaidi kwa sababu tumeshusha kazi hii ifanywe sasa na Halmashauri za Wilaya, Mkuu wa Wilaya na Kamati yake ya Ulinzi na Usalama anaweza kuhusisha mpaka Watendaji wa Kata ili kuwatambua wakulima waliolima kiwango kikubwa cha korosho. Kwa hiyo, kazi hiyo inaendelea vizuri. Ahsante sana. (Makofi)