Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka (5 total)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Nina swali moja kwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tangu napata ufahamu kulikuwa na sera katika nchi yetu ya wataalam, wafanyakazi wale wa nje, zamani walikuwa wanaitwa ma-TX. Wafanyakazi wa nje, kulikuwa na sera kwamba wanafanya kazi kwa kupata kibali kutoka uhamiaji cha miaka miwili, wakitegemewa kwamba kipindi hicho wana-recruit Mtanzania kwenye kampuni au kwenye kiwanda hicho na baada ya miaka miwili tunatarajia kwamba yule TX atakuwa ameshamhitimisha yule kijana au yule mfanyakazi atakuwa amehitimu na kibali chake kitakoma. Kama huo ujuzi utakuwa bado unahitajika, yaani hapana mtu aliyehitimu, ataongezewa tena miaka miwili kutimiza miaka minne. Je, Mheshimiwa Waziri Mkuu, hiyo sera bado ipo? Kama ipo, bado inatekelezwa?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme kwamba, sera ile bado ipo na Serikali tunaisimamia. Msingi wa jambo hili wa kuwapa muda mfupi hawa watalaam wenye ufundi maalum nchini kwetu katika sekta za kazi, ilikuwa ni kujenga wigo mpana kwa Watanzania kupata ajira na kuweza kusimamia maeneo haya ambayo yanahitaji pia utalaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumefanya hili kutoa nafasi kwa watumishi wa nchi za nje kuja nchini Tanzania kufanya kazi ambazo hapa ndani tunakosa utalaam; ndiyo tunapofuata utaratibu huo. Tunawapa miaka miwili ya kwanza, tukiamini kwamba Watanzania waambata watakuwa wameshajifunza utalaam ule na baada ya miaka miwili wanaweza kuondoka. Pale ambapo inaonekana kuna uhitaji zaidi, sheria inawaruhusu kuwaongezea miaka miwili ili tuendelee, lakini mwisho tunaweza kumwongezea mwaka mmoja na kufanya miaka mitano ya mwisho. Baada ya hapo, tunaamini Watanzania watakuwa wameshaweza kupata ile taaluma na kusimamia sekta za kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka niwahakikishie, mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba tunafungua milango ya ajira kwenye sekta zote ikiwemo na utaalam, tutaendelea kuusimamia utaratibu huu wa kupokea watalaam kutoka nje wenye utalaam ambao nchini kwetu haupo ili kutoa nafasi kwa Watanzania kujifunza na baada ya miaka miwili tutataka wale wa kutoka nje warudi nchini kwao ili nafasi zile ziendelee kushikiliwa na Watanzania. Tutaendelea kusimamia Mheshimiwa Mbunge.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kumuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nchi yetu imekuwa na sera nyingi sana, sera ambazo mara nyingi utekelezaji wake ama ni pungufu au hazitekelezwi kabisa. Sera hizi mara zote kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi zimekuwa zikirudiwa rudiwa mara nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo swali langu litaenda kwenye Sera ya Maji ya mwaka 1991 ambayo lengo kubwa ilikuwa wananchi wetu waweze kupata maji kwa umbali wa mita 400, utekelezaji wa sera hii mpaka ifikapo mwaka 2002, siyo hivyo tu, Julai 2002 hiyo baada ya ile sera kuwa haijafikiwa, ikafanyiwa mapitio tena, ikatambua kwamba maji ni uhai, maji ni siasa, maji ni uchumi, vilevile ikaingizwa rasimu ya kwamba maji na mazingira.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, mpaka leo hii wananchi wetu wamekuwa na janga kubwa la maji. Ni nini kauli ya Serikali juu ya utekelezaji wa sera hii?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri kwamba sera hiyo tunayo na huo ndiyo msisitizo wetu na hata bajeti ambazo Waheshimiwa Wabunge huwa mnazipitia kila mwaka zinalenga kufikia hatua hiyo. Nataka niwahakikishie kwamba pamoja na mipango ya Serikali ya usambazaji wa maji, pamoja na kutenga bajeti ambazo tunazo huku ndani, bado tunapata tatizo kubwa nchini la kupatikana kwa vyanzo vya kutosha vya maji vinavyoweza kutosheleza kusambaza maji kwa kiwango ambacho tumejiwekea.

Mheshimiwa Naibu Spika, sera ni malengo na malengo yetu tunataka tuyafikie, tunapata changamoto kwenye utekelezaji kama ambavyo nimeeleza. Sasa hivi nchi imekumbwa na uharibifu mkubwa sana wa mazingira na nimelieleza mara kadhaa. Maeneo haya yamesababisha kukosekana upatikanaji wa maji na miradi mingi ambayo inatakiwa itekelezwe ni ya gharama kubwa kwa sababu inatakiwa tufuate maji kwenye umbali mkubwa ambapo gharama zake ni kubwa, hiyo sasa inakuja kugongana na mahitaji pia ya bajeti. Waheshimiwa Wabunge sasa hivi tuko kwenye Bajeti ya Maji ambayo mnaendelea kujadili na kushauri Serikali na Serikali kwa usikivu tulionao tutaendelea kuwasikiliza na kuyachukua yale yote muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kutumia nafasi hii kuwasihi Waheshimiwa Wabunge tushirikiane sana katika kuhakikisha mazingira yetu nchini yanalindwa ili tuwe na vyanzo vya kutosha, Serikali imudu kuchimba visima hata vya urefu wa kati au urefu mfupi ili kuweza kumudu kusambaza maji kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo kubwa ambalo tunalipata sasa ni hilo la kukosekana kwa vyanzo sahihi vya maji. Lakini pia nitumie nafasi hii kuwasihi Watanzania, tuendelee kuvitunza vyanzo vyetu vya maji ili Serikali isitumie gharama kubwa kutafuta mradi ambao maji yake hayatoshi na kama unayapata ni ya muda mfupi kwa sababu huku juu kote kuko kweupe na jua linavyopiga maji yote hukauka.

Kwa hiyo, nataka nikuhakikishie kwamba Ilani yetu inayosema katika kipindi cha miaka mitano tunataka tufikie hatua fulani, tutaitekeleza. Serikali ya Awamu ya Tano sasa tuna mwaka mmoja na tunaomba ridhaa yenu mwaka wa pili wa utekelezaji, mpaka kufikia mwaka 2020 kama miaka mitano ya ahadi zetu, tunatarajia sehemu kubwa ya nchi kwenye vijiji, kata na miji mikubwa tuwe tunapata maji kwa kiwango ambacho tumejiwekea commitment kwenye sera ya kufikia mita 400 kila mmoja aweze kupata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumemuona Makamu wetu wa Rais, Mama Samia Suluhu akipita kuzindua miradi mingi sana, naomba sasa mtupitishie bajeti yetu ambayo tunaijadili hapa ili tuendelee kutoa huduma za maji. Tunajua tuna changamoto, inaweza kuwa fedha kidogo lakini tutaendelea kuwa na miradi mingi sana ambayo tutaifungua. Juzi tumefungua mradi mkubwa sana Tabora, unaotoa maji Shinyanga, Ziwa Victoria, tunasambaza Tabora na Wilaya zake zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea na miradi mikubwa kama hiyo, tutaendelea kuzungumza na marafiki zetu ambao pia tunapata miradi ili tuweze kusambaza miradi hii kwenye vijiji na kwenye umbali ambao tumeuweka kwenye sera yetu. Ahsante sana.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu hapa nchini tunazo Sera za Ugatuaji wa Madaraka. Hii Sera ya Ugatuaji wa Madaraka lengo ilikuwa ni kufikisha huduma hizi kwa jamii kwa karibu zaidi na usimamizi wa karibu wa miradi yetu ya maendeleo inayoibuliwa katika Halmashauri zetu na vijiji.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, ili sera hii iweze kutekelezwa ni kwamba Serikali inapeleka pesa nyingi kwenye Halmashauri zetu ili kuweza kutekeleza miradi hiyo na kutoa hizo huduma. Hata hivyo, kada hii, wasimamizi wakubwa wa kwanza kabisa wa fedha hizi ambazo Serikali tunapeleka ni Watendaji wetu wa Vijiji na Watendaji wa Kata.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, sasa hivi nchi yetu inakumbwa na tatizo kubwa sana katika Halmashauri zetu kutokana na uhaba wa Watendaji wa Kata na Watendaji wa Vijiji wakati hao ndiyo tunaowategemea kwamba ndiyo wangekuwa wasimamizi wa kwanza wa fedha hizi.

wali langu ni kwamba mkakati wa Serikali ya Awamu ta Tano unasema nini katika kutatua tatizo hili ambalo limekuwa sugu, linasababisha Halmashauri zetu kupata hati isiyo salama?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka ambalo limezunguka zunguka lakini msingi wake ni Serikali inatumia utaratibu gani kuhakikisha kwamba kunakuwepo na rasilimali watu ambao pia wataweza kudhibiti rasilimali fedha kama ambavyo nimekuelewa kwa mzunguko mzima wa swali lako.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imeweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba tunakuwa na watumishi wa kutosha kwenye kada zote. Kwa sasa tunaendelea kushuhudia kupungua kwa rasilimali watu kwenye sekta zetu na hatimaye kusababisha rasilimali fedha hizo kutotunzwa/ kutosimamiwa vizuri. Kwa Serikali ya Awamu ya Tano, jambo hilo linaweza kuwa limetokana na mazoezi mawili ambayo tumeyaendesha; ya kubaini watumishi hewa na watumishi wenye vyeti ambao hawana stahili sahihi ya kufanya kazi walioajiriwa. Sasa zoezi hili limepunguza idadi ya watumishi na ni kweli kwamba tunaweza tukawa tunapeleka fedha halafu zisipate watu wa kuzisimamia vizuri.

Mheshimiwa Spika, kwenye eno hili, Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli ametupa nafasi za ajira zaidi ya 52,000 na tumeanza kuajiri kwa sababu anatupa vibali kadiri tunavyohitaji na tunaendelea kuhakiki kwamba wanaokwenda ni watumishi wenyewe na wamefika vituoni wanafanya kazi yao. Kama ambavyo mmeshuhudia tumeajiri kwenye Sekta ya Elimu, Afya na juzi Majeshi na tunaendelea kuajiri.

Mheshimiwa Spika, sasa kada hizi za Watendaji wa Kata na Vijiji hizi ni kada ambazo pia tumezipa mamlaka halmashauri zenyewe kuajiri pale ambapo wanaona kuna upungufu ili kuziba mapengo haya. Kwa hiyo ni halmashauri yako na Mheshimiwa Mbunge wewe pia ni Mjumbe wa Baraza la Madiwnai pale, kwa hiyo unayo fursa ya kupata takwimu za Watendaji wa Kata na Vijiji waliopo na kujua wangapi wamepungua ili muamue na muweze kuziba ninyi wenyewe pale kwa lengo la kuweza kudhibiti fedha zilizopo na zilizopelekwa kwa ajili ya miradi kwenye ngazi hizo za vijiji.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi kuuliza swali kwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na songombingo iliyoipelekea zao la korosho kwa msimu uliopita ambao sasa hivi tunaendelea nao kukosa soko jambo lililopelekea Serikali kuingilia kati na kutangaza kwamba inakwenda kununua korosho za wakulima. Hata hivyo, hadi leo wakulima walio wengi hawajapata fedha zao wakati korosho tayari zimeshachukuliwa na Serikali. Siyo hivyo tu, kuna baadhi ya wakulima wameanza kulipwa kidogo kidogo lakini kinachoshangaza wakulima wengi wanalipwa Sh. 2,600 kwa kilo kinyume na Mheshimiwa Rais alivyotangaza kwamba korosho anakwenda kuzinunua kwa Sh. 3,300 kwa kilo.

Mheshimiwa Spika, nini kauli ya Serikali kulingana na hii sarakasi inayoendelea sasa hivi kwenye zao hili la korosho? Kwa sababu sasa hivi msimu wenyewe unakwenda kuisha lakini wakulima malalamiko ni makubwa sana? Nini kauli ya Serikali? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshiiwa Spika, katika kipindi hiki cha Bunge cha wiki mbili hizi suala la korosho limezungumzwa sana na Wizara kwa maana Serikali imetoa ufafanuzi sana namna ambavyo tunaendelea kufanya malipo ya zao la korosho kwa wakulima wanaolima zao hili walioko kwenye mikoa hii mitano ya Ruvuma, Mtwara, Lindi, Pwani na Tanga ambako sasa wako kwenye masoko. Tunachosema zao la korosho siyo kwamba lilikosa soko bali lilikosa bei nzuri, wanunuzi wapo lakini lilikosa bei nzuri. Pale ambapo wanunuzi walikuwa wananua kwa bei ya chini sana kuliko hata ile bei ya kwenye soko la dunia na ilikuwa haimletei faida mkulima. Kwa nia nzuri ya Mheshimiwa Rais akaamua korosho hizi sasa tutanunua kwa Sh.3,300 bila makato yoyote yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alipotoa kauli sasa Bodi ya Mazao Mchanganyiko yenye dhamana kisheria ya kununua mazao na kutafuta masoko popote pale na hasa kwa mazao ambayo yanaonekana yanasuasua kupata masoko ilianza kazi yake. Imetafuta fedha, baada ya kufanya tathmini ilishajua kiwango cha korosho kitakachozalishwa na gharama zake, wana uwezo nalo, wameanza kazi hiyo na sasa wanaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tamko la Mheshimiwa Rais kununua kwa Sh.3,300 kwa kilo maana yake anazungumzia standard grade ile bei kwa korosho ya daraja la kwanza. Zao la korosho lina grade I, II, iko sheria inayoongoza Bodi ya Korosho kwamba korosho za daraja la II zitauzwa asilimia 80 ya bei ya daraja la I. Kwa hiyo, bei iliyotamkwa ni ya daraja la I, unapokuwa na korosho daraja la II maana yake sasa unarudi kwenye sheria yetu mkulima huyu atalipwa kwa bei ya daraja la II ile asilimia 80 ya bei ya daraja la I. Kwa hiyo, ndicho ambacho kinafanyika, hiyo Sh.2,600 ni calculation ya asilimia 80 ya bei ya daraja la I. (Makofi)

Mheshimiwa Spoika, lakini malipo haya yanaendelea vizuri na kama vile tulijua swali litakuja tena na wakati wote kwa kuwa timu iliyoko kule Mtwara inaendelea kutoa taarifa mpaka jana tumewaongezea tena shilingi bilioni 100 na sasa inafanya zaidi ya shilingi bilioni 500 kulipa na mahitaji yetu sisi ni shilingi bilioni 700. Kwa hiyo, wakishamaliza tunaongeza na kuhakikisha tunamaliza na kama ambavyo unajua niliingilia kati mchakato mzima na kuwapa tarehe ya mwisho ya kulipa wakulima ambayo ni tarehe 15, tuna uhakika kufikia siku hiyo tutakuwa tumefikia kiasi kikubwa cha malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka niwahakikishie wakulima kwamba malipo yanaendelea na sehemu kubwa ya wakulima tumeendelea kuwalipa na hasa wale walioko chini ya kilo 1,500 lakini sehemu kubwa ya malipo ambayo yanakuja sasa ni wale wa zaidi ya kilo 1,500, uhakiki umeshafanyika na wanatambulika na sasa utaratibu wa kulipa ambao unaendelea ndiyo ambao utawafanya wakulima sasa kila mmoja aweze kupata fedha yake. Nataka niwahakikishie wanunuzi wa korosho na wakulima wa korosho kwamba korosho zote kama ambavyo tumetamka mara zote kwamba tutazinunua kama ambavyo imekubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini taratibu zinazoendelea ni ili tujue kwa uhakika zaidi mkulima anayelipwa kuwa ndiye mwenye mali na ndiyo anayelipwa, huo ndiyo mkakati ambao unaendelea kwa sasa. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge wenzangu na hasa mnaotoka kwenye maeneo ya korosho muwe na amani kabisa, Serikali inaendelea na utaratibu wa kulipa na tutawalipa wakulima wote kwenye maeneo yote. Wakulima wenyewe wawe na imani na Serikali yao na mpango ambao unaendelea kwamba kila mkulima aliyepima korosho zake atafikiwa na atapata malipo yake. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kwanza kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, swali langu litahusu sekta ya korosho. Mwaka huu tumepata taarifa kwamba Serikali ilijipanga kutupatia pembejeo wakulima wa zao la korosho kwa maana kwamba waje kuzilipa baadaye kwenye mjengeko wa bei. Hata hivyo, kuna taharuki kubwa kwa wakulima wetu wa korosho baada ya Bodi ya Korosho kuleta waraka kwenye Halmashauri zetu, wakiwaambia kila mkulima akipeleka zao lile kwenye mnada kila kilo moja itakatwa shilingi 110 bila kujali kwamba mkulima yule amechukua pembejeo kwa kiwango gani. Barua ile inasema kwamba jambo hili hata sisi Wabunge tumeliridhia.

Mheshimiwa Spika, sasa kuna taharuki kubwa sana kiasi kwamba mpaka…

SPIKA: Swali lako ni nini katika jambo hilo?

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, kutokana na mkanganyiko huu ni nini kauli ya Serikali ili wakulima wetu waendelee kuchukua zile pembejeo maana sasa hivi wanaziogopa.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Wizara yetu ya Kilimo imetoa miongozo kadhaa ya kuboresha masoko ya mazao nchini ili kuwanufaisha wakulima kwenye mazao wanayoyalima ikiwemo na kuwarahisishia namna nzuri ya kupata pembejeo. Zao la korosho ni miongoni mwa mazao ambayo Serikali kupitia Wizara ya Kilimo imeendelea kufanya mapitio ya maboresho ya namna nzuri ambayo wakulima ambao kwa sasa ndiyo wapo kwenye msimu wa kutumia pembejeo ili waweze kupata pembejeo wakulima wote na waweze kushiriki vizuri kwenye kilimo hiki.

Mheshimiwa Spika, nakiri kwamba ipo taharuki kwa sababu na mimi ni mdau pia wa zao hilo lakini taharuki hii imetokana na vikao vya awali vya majadiliano ya mfumo mzuri ambao pia wakulima nao wanaweza kushiriki vizuri kupata pembejeo. Si kwamba Wabunge wameshiriki katika kutoa maamuzi, hapana, bali Wizara inaendelea kuwa na vikao vya mara kwa mara ili kufikia hatua nzuri ya kuwezesha kila mkulima kupata pembejeo. Vikao hivi bado havijakamilika na kikao kikubwa kabisa kipo tarehe 6 ambacho kinaalika wakulima, viongozi wa ushirika, viongozi wa Serikali na Waheshimiwa Wabunge pia mtaalikwa ambacho sasa tutajadili namna nzuri ya kumwezesha mkulima kupata pembejeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maelekezo ya awali ya kwamba kila mkulima atakatwa shilingi 110 yamesitishwa kwa muda ila wakulima wote waende kupata pembejeo zile ambazo zimepelekwa kwenye maeneo yale. Kiwango cha pembejeo kilichoagizwa kinatosha kabisa kwa kila mkulima kutokana na takwimu zilizopatikana kutoka vyama vyetu vya ushirika ili kila mkulima apate pembejeo ya kutosha kupuliza awamu zote nne kufikia kipindi cha uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kikao kile cha tarehe 6 ndicho kitakachotoa mwelekeo mzuri wa nini kitafanyika kwa pembejeo ambazo zimetolewa na wala haitakuwa kumkata kila mkulima kwa kilo aliyoipeleka sokoni kwa sababu wapo wengine wana kilo mbili, wengine kilo 10 lakini wapo wamezalisha zaidi ya tani 20, sasa huwezi kukata kwa kila kilo. Kwa hiyo, hilo linafanyiwa kazi na Wizara na ufafanuzi utatolewa siku ya tarehe 6 ambapo wadau wa zao la korosho kila mmoja atashiriki kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwasihi wakulima wa zao la korosho waendelee kupokea pembejeo zile. Serikali inaendelea kuangalia namna bora ya kumfanya mkulima aweze kupata pembejeo kwa gharama nafuu ili aweze kuendelea kulima zao hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niongezee eneo lingine ambalo pia limeleta mkanganyiko kwamba mabenki ambayo miaka yote yamekuwa yakitoa mikopo kwa wakulima, mwaka huu walisimama kutoa mikopo yao kwa hofu kwamba wakulima watakapopata pembejeo huku Serikalini hawataweza kulipa gharama ya mikopo ambayo wameikopa kwenye mabenki. Tumeruhusu mabenki yaendelee kukopesha wakulima kwa sababu bado kwenye zao la korosho kuna shughuli nyingi za kufanya; pamoja na kupilizia dawa lakini pia kuna kupalilia, kuokota na kuhakikisha zao linakwenda sokoni, yote inahitaji mtaji ambapo mkulima ambaye amelima, anajiamini kwamba atakopa na kurejesha, bado mabenki yaendelee kukopesha. Tumeshawapa maelezo hayo mabenki na wanaendelea na kukopesha. Kwa hiyo, wakulima waende wakakope kulingana na mahitaji yake ili alihudumie zao na hatimaye aweze kurejesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuwaambia Waheshimiwa Wabunge wote wanaotoka kwenye majimbo yanayolima zao la korosho muendelee kuiamini Serikali na mifumo ambayo inaendelea kuipanga. Mifumo hii haiamuliwi tu moja kwa moja na Serikali bali inashirikisha wadau na kwa zao la korosho wadau tutakutana siku ya tarehe 6. Kwa hiyo, siku hiyo tutatoa mwelekeo wa zao hilo sote kwa Pamoja. Kwa hiyo, wawe na amani na waendelee na uratibu wa zao hili la korosho, ahsante sana. (Makofi)