Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Jacqueline Kandidus Ngonyani (Msongozi) (41 total)

MHE. JAQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ambayo kimsingi sijaridhishwa nayo ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo, nina maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Ruvuma una wakazi zaidi ya watu 150,000 na ruzuku/vocha zinazotolewa kwa maana ya pembejeo za kilimo ni karibu kwa watu 80,000 ni wazi kuwa hazikidhi haja. Swali langu, naomba anieleze leo ni lini Serikali itaondoa angalau ushuru kwa maana ya cess kwa wakulima ili pale wanapotoa mazao yao shambani wasitozwe tozo yoyote ile?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, mawakala wa pembejeo za kilimo ambao wamehudumia kwa maana ya kuikopesha Serikali kwa msimu wa mwaka 2015/2016 mpaka sasa hawajalipwa pesa zao. Naomba Waziri anipe majibu mazuri na ya kina kwamba ni lini Serikali itawalipa mawakala hawa ambao wamehudumia wananchi katika Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Ruvuma za Nyasa, Mbinga, Songea, Namtumbo pamoja na Ruvuma ikiwepo pia hata maeneo mengine yote ya nchi yetu ya Tanzania? Hawa watu wanafanya biashara kwa kukopa kwenye benki na sasa hivi imefika mahali wanashindwa kurejesha mikopo yao. Naomba anipe majibu ya kina.
NAIBU WAZIRI KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ni lini Serikali itaondoa ushuru, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Finance Bill inayotegemewa kuja katika Bunge hili tumependekeza kwa Wizara ya Fedha, baadhi ya hizo tozo ziondolewe. Kwa hiyo, tunategemea tutakapoleta Waheshimiwa Wabunge mtatuunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nieleze tu kwamba kuna tozo nyingi ambazo zimekuwa zikiongeza bei ya pembejeo kwenye mjengeko wa jumla ambazo nyingi kwa kweli zinaleta matatizo kwa wakulima na tutahakikisha nyingi zitaondolewa. Vilevile tufahamu kwamba suala la kodi ni la kisheria, kwa hiyo, kuna baadhi ya kodi ambazo tutaziondoa taratibu lakini kimsingi Wizara yangu ipo kwenye utaratibu mzima wa kuhakikisha kwamba baadhi ya hizi kodi zinaondoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili la mawakala ambao hawajalipwa, nikiri kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna mawakala ambao hawajalipwa mpaka sasa. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kuwa tayari Wizara imejipanga kuhakikisha kwamba tunamaliza madeni yote ya mawakala ili wasiendelee kupata vikwazo kama wanavyopata, wengi wanauziwa mali zao kutokana na mikopo. Tunawasihi mawakala wote wapeleke certificate zao kwa sababu tayari utaratibu wa kuwalipa unaandaliwa. Nashukuru sana.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Kwanza, Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa mikoa yenye wananchi wengi sana na katika vijiji ambavyovimeainishwa kwa ajili ya kupewa mikopo hiyo, kila kijiji kina wastani wa wananchi 5,000 ambao wana uwezo wa kufanya kazi za uzalishaji. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapa mikopo yenye tija wananchi hao?
Swali la pili, kama wanakijiji watapata shilingi 1,000 kila mmoja itakayotokana na shilingi milioni 50. Je, watawekeza kwenye biashara gani ili wapate faida kwenye uwekezaji huo?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WALEMAVU): Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kumpongeza sana huyu Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Ruvuma kwa kazi nzuri na jitihada kubwa anayoifanya ya uwakilishi ndani ya Bunge na hasa kuwawakilisha Watanzania wote, lakini hasa hasa wanawake wa Mkoa wa Ruvuma nampongeza sana. Mheshimiwa Mbunge ameniuliza maswali mawili la kwanza ameonyesha idadi ya watu jinsi ilivyo, katika maeneo mbalimbali kwenye Vijiji vya Mkoa wa Ruvuma, akitaka kujua kama tuna mpango mahususi katika Serikali wa kuhakikisha vijiji hivyo vinapata mikopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, wakati tukipitisha bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, Fungu 65 mradi namba 49, 45 pamoja na hiyo milioni 50. Hata hivyo, Serikali imetenga fedha nyingine bilioni moja kwa ajili ya kuhakikisha kwamba vijana na akina mama wanapata mikopo katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania. Hata hivyo, Serikali pia kupitia Halmashauri zetu itaendelea kutenga asilimia tano ya mapato kwa ajili ya akinamama na vijana. Kwa hiyo, namhakikishia kwamba nguvu hizo zote zitasaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili la nyongeza amesema, pia anakadiria wastani wa shilingi 1,000 kama Mfuko huo utakopeshwa kwa wananchi, kwa idadi ya wananchi ambao wanaweza kuifanyia kazi. Namwomba Mheshimiwa Mbunge asubiri kama nilivyosema, tunatengeneza utaratibu na mfumo mzuri ambao utasaidia kuhakikisha kwamba wakopaji watapata fedha yenye tija na wataweza kufanya kazi na biashara ambazo zitainua kipato kwa familia zao na Taifa zima kwa ujumla.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, tatizo la mradi wa umwagiliaji la Mufindi Kaskazini linafanana kabisa na tatizo la mradi wa umwagiliaji uliopo katika Halmashauri ya Songea katika Kata ya Subira na katika Mtaa wa Subira. Mradi huu ni
wa muda mrefu, umeanza tangu mwaka 2008 na mpaka sasa hivi bado haujakamilika, pesa zilizotumika mpaka sasa hivi ni shilingi milioni 585 na bado panatakiwa zaidi ya shilingi bilioni moja ili kukamilisha mradi huu. Je, Serikali imetenga kiasi gani kwa ajili ya kukamilisha mradi huu kwa kipindi hiki cha Bajeti ya mwaka 2017/2018?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli miradi mingi ya umwagiliaji ina matatizo. Na ina matatizo kwa sababu, kwanza kulikuwa na udhaifu katika usimamiaji katika sekta hii, hii miradi ya kilimo. Na miradi mingi ilikuwa ina ufadhili wa JICA. Kwa hiyo, kulikuwa na weakness katika usimamizi, yaani ulikuwa dhaifu na ndio maana utekelezaji wake haukwenda kwenye viwango vinavyotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nikiri tu kwamba katika bajeti ya mwaka huu wa fedha tulitenga fedha kwa ajili ya kufanyia mapitio ya miradi yote ya umwagiliaji, ili kwanza tuweze kuirekebisha iweze kufanya kazi iliyokusudiwa, hiyo ndio kazi ambayo inaendelea sasa hivi.
Lakini pili, tulikuwa tunafanya usanifu wa miradi mipya ya umwagiliaji, sasa kwa sasahivi siwezi kukwambia bajeti ya mwaka 2017 ni kiasi gani, lakini nitakapowasilisha bajeti yangu najua utaunga mkono ili kusudi tuweze kukamilisha huu mradi wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kw amajibu mazuri. Pamoja na majibu mazuri hayo napenda kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utekelezaji huu bado kuna maeneo mbalimbali katika Halmashauri mbalimbali katika Mkoa wangu wa Ruvuma na maeneo mengine kwenye Halmashauri nyingine maeneo mbalimbali ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ina mpango gani wa kuwachukulia hatua kali halmashauri ambazo bado wanawanyonya kwa kuwatoza ushuru wajasiriamali wadogo wadogo wote katika Halmashauri zote zilizoko mkoani Ruvuma na maeneo mengine? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa wafanyabiashara hao wadogo wadogo wanafanya biashara katika mazingira magumu sana jua la kwao, mvua ya kwao, vumbi lao. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwawekea mazingira bora ili wamachinga hao waweze kuepuka adha hiyo wanayoipata? (Makofi
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi sote ni mashuhuda kwamba, Sheria hii ilipitishwa na Bunge lako Tukufu na kwa vyovyote vile hakuna kisingizio chochote ambacho kinaweza kikatolewa na halmashauri eti kwa sababu, wakidhani kwamba, sheria ndogo ambazo wao hawajazipitisha zinakuwa zinakinzana kwamba hazitawaletea mapato. Naomba niwasihi Wakurugenzi wote Halmashauri zote, na jambo hili hata Mheshimiwa Rais amekuwa akilirudia, naomba niliseme kwa mara ya mwisho; Mkurugenzi yeyote wa halmashauri iwayo yoyote ambaye atapingana na maelekezo haya na sheria aambayo imetungwa na Bunge lako Tukufu, sisi kama Serikali hatutasita kumchukulia hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili anaulizia namna ya kuwawekea mazingira mazuri wafanyabiashara wadogo wadogo. Ni dhamira ya Serikali na ndio maana tunaanza kwa kuwatambua kwa kuwapa vitambulisho ili tuhakikishe kwamba, wanatengewa maeneo mazuri ili wafanye kazi katika mazingira yaliyo mazuri kwa ajili ya kuongeza kipato cha nchi.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyoko katika Jimbo la Manonga linafanana kabisa na changamoto iliyoko katika mkoa wangu wa Ruvuma. Katika mkoa wa Ruvuma kuna changamoto ambayo itaenda sambamba na tatizo la kubadili mita za maji kutokana na mfumo wa kupata maji kwa maana ya mita ibadilike kuwa wananchi wapate maji kwa mfumo wa unit. Sambamba na hilo, iko miradi ambayo nilikuwa nikisema hapa mara nyingi katika mkoa wangu wa Ruvuma ambayo kimsingi inaonekana kwamba imekamilika laikini haitoi maji, na miradi hiyo inataokana na World Bank.
Mheshimiwa Mwenyekiti, World Bank wamefanya hiyo kazi na miradi inaonekana kwamba sasa tayari inatoa maji, lakini katika miradi hiyo kuna mradi wa maji wa Mkako (Mbinga), Ruhuwiko (Songea Mjini), Matemanga na Ndembo (Tunduru), Litola (Namtumbo)...
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango gani ya kuhakikisha miradi hii inafanyiwa marekebisho ili iweze kutoa maji na wananchi waweze kufaidika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema kwamba miradi imekamilika lakini maji haitoi kwa wananchi. Lengo la Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji na fedha zimetolewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ile. Lakini cha kushangaza miradi imekamilika haitoi maji. Labda nimuombe Mheshimiwa Jacqueline kwamba baada ya Bunge tuongozane pamoja tukaone sababu gani zinazosababisha mradi ukamilike lakini hazitoi maji? Kama kuna mtu ambaye anasababisha au kukwamisha ili maji isitoe tutalala naye mbele ili wananchi wetu waweze kupata maji.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa tatizo la gati lililopo katika Wilaya ya Geita linafanana kabisa na tatizo la gati lililoko katika Wilaya ya Nyasa. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Gati ya Ngumbi katika Ziwa Nyasa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, samahani nadhani ni Ndumbi.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO:Mheshimiwa Naibu Spika, gati linaloongelewa kama ambavyo mmeona linamuhusu sana Naibu Waziri anayehusika na masuala ya Elimu; na kwa kweli nilishuhudia mwenyewe wakati nilipoenda kukagua ile gati ambayo inatumika kupakia mkaa wa kutoka Ngaka kwamba tunahitaji kufanya mambo mazito pale ili ile biashara ambayo tayari imeshapanuka iweze kufanyika kikamilifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, anafahamu Mheshimiwa Naibu Waziri na Mheshimiwa Jacqueline Msongozi kwamba katika bajeti hii ambayo nawashukuruni sana Waheshimiwa Wabunge; na mnisamehe jana nilipa matatizo kidogo kuona kwamba mmeniwezesha kuanza kujenga reli na miundombinu mingine nikatoa kwa sauti kubwa sana kuunga mkono bajeti, nanyi mkapitisha; pamoja na hii gati ambayo ipo ina bajeti tutaisimamia kuhakikisha inakamilika na kile tunachokusudia kitendeke pale Ndumbi kiweze kukamilika.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Nakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumuuliza Waziri wa Maji, kumekuwa na miradi ya World Bank ambayo ilianza mwaka 2013 na miradi hii baadhi yake huwa inatolewa ripoti kwamba tayari imekamilika ilhali maji hayatoki katika maeneo hayo. Napenda kuainisha maeneo ambayo maji hayatoki ikiwa ni pamoja na kumwomba Waziri mwenye dhamana akubaliane nami baada ya Bunge hili twende pamoja kwenye maeneo hayo ili akajionee yeye mwenyewe adha ambayo wanaipata wanawake kuhusiana na miradi hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya ni yafuatayo: Litola na Kumbara ni baadhi tu ya maeneo katika Wilaya ya Namtumbo; Wilaya ya Mbinga kuna mradi wa Mkako na Litoha; Wilaya ya Tunduru kuna Nanembo na Lukumbule; lakini pia katika Manispaa ya Songea kupitia SOWASA Kata ya Ruvuma, Subira, Luwiko, Bombambili, Msamala na Matalawe ni maeneo ambayo maji hayapatikani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ningependa baada ya Bunge hili tuweze kuongozana akaone mwenyewe kwa macho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili…
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Nahitaji Waziri niongozane na yeye akaone mwenyewe.
Swali la pili, katika Kituo cha Afya cha Lipalamba hakuna maji kabisa na wananchi sasa wameshaanza kujichangisha kwa ajili ya kuchimba mitaro kwa ajili ya kutandika mipira ya mabomba. Je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kutoa fedha kwa ajili ya kununua roll mita 30 kwa ajili ya kutandika pamoja na vifaa vyake vya kuungia?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ameomba kama niko tayari kuongoza naye kwenda kuona maendeleo ya utoaji wa huduma ya maji katika Mkoa wa Ruvuma. Nakubali ombi lake, nitafanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili na katika jibu la msingi, tumesema kweli katika vijiji 80 vipo vijiji ambavyo bado miradi haijakamilika na kwamba iko katika hatua mbalimbali. Sasa kuwa na jibu ambalo ni mahususi kujua kijiji gani tumesema imekamilika na maji hayatoki, hii inabidi tuifanyie verification. Haya majibu yanayoletwa inawezekana yakawa sio sahihi, lakini naomba sana Waheshimiwa Wabunge katika vikao vya Halmashauri za Wilaya taarifa hizi za maendeleo ya huduma za maji katika maeneo yale huwa zinatolewa kila robo mwaka, naomba sana tuwe tunahudhuria vikao vile ili tuweze kujua.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kama kuna tatizo la msingi la kisera ambalo Waziri inabidi nijue, naomba Mheshimiwa Mbunge tuendelee kuwasiliana ili tuweze kuona namna gani tutamaliza matatizo ya maji kwa wananchi wetu.
MHE. JAQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza yenye seheu (a) na (b).
Mheshimiwa Mwenyekiti, ubora wa tumbaku unategemea sana upatikanaji wa mbegu, mbolea, madawa kwa wakati muafaka. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha pembejeo zinawafikia wakulima kwa wakati unaotakiwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni nini faida na hasara ya kumruhusu mnunuzi kupeleka mbolea kwa wakulima?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kama inavyofahamika kwamba zao hili la tumbaku limekuwa na mchango mkubwa sana katika uchumi wa nchi yetu. Kwa misingi hiyo, Serikali imekuwa ikijitahidi kuhakikisha kwamba pembejeo zinapatikana na zinawafikia walengwa kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nini tatizo la kumfanya mnunuzi aweze yeye kupeleka mbolea. Mnunuzi mzuri anapopeleka mbolea kwa tija ili mwananchi huyu apate hiyo mbolea kwa tija huwa hakuna tatizo lakini kuna wanunuzi ambao ni wanyonyaji ambao wanapeleka mbolea na kumwambia mwananchi kwamba ukishapata hii mbolea yangu na mazao yako yote lazima uniuzie mimi kwa bei anayoitaka yeye, huo ni unyonyaji na mnunuzi wa aina hiyo huwa tunakuwa hatumtaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndiyo maana sasa hivi kupitia maagizo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa, katika mazao makuu matano ya nchi hii yanawekewa utaratibu maalum ili kuhakikisha kwamba vyama vya ushirika viwe na nguvu na kusaidia kuwawezesha wananchi ili wasiendelee kunyonywa.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sera ya Serikali ni kuhakikisha kwamba Wazee wanapata matibabu bure na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya afya na Naibu wake, wamesisitiza kwamba Wakurugenzi waendelee kutoa kadi za Bima ya Afya kwa wazee wasiojiweza ili waweze kupata matibabu lakini hawa wazee kupewa Kadi ya Bima ya Afya tu siyo dawa tosha, endapo kama vituo vya afya watakavyokuwa wanaenda kutibiwa hawatapata dawa na vifaa tiba.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba inamaliza kabisa tatizo la upungufu wa dawa pamoja na vifaa tiba ili wazee hawa waepukane na kadhia ambayo wanaipata pindi wanapokwenda kutibiwa katika vituo vya afya katika Mkoa wote wa Ruvuma?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati ya kutosha tunayo ya kuhakikisha tunaboresha huduma za afya nchini. Tuna mkakati wa miaka mitano wa kutoa huduma za afya nchini yaani Health Sector Strategic Plan 2015-2020) na mle ndani tumeelekeza kila kitu. Kwa bahati mbaya sana hatuna uwezo tu wa kiuchumi wa kuweza kuutekeleza mpango ule kwa asilimia mia lakini tunajitahidi. Kwa mfano kwenye ule mpango, tungetakiwa kwa mwaka kwenye bajeti ya afya peke yake tutenge shilingi trilioni 4.5 ambayo imeandikwa katika ule mpango mkakati wa afya wa miaka mitano lakini sisi tuna uwezo wa kutenga shilingi trilioni 2.2. Kwa hivyo, lazima utaona kutakuwa na upungufu tu kwa sababu kadri tulivyotazama mbele kama nchi hatujaweza kufikia pale ambapo tunatamani kufika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu kwamba tuna suluhu ambayo ni kuanzisha Bima ya Afya ya lazima kwa kila Mtanzania. Kwa sababu Bima ya Afya ya lazima kwa kila mtu maana yake ni kwamba kila mtu atakuwa amechangia kiasi fulani kwenye mfuko wa kutolea huduma za afya lakini siyo watu wote watakaougua maana yeke zile pesa ambazo kila mmoja wetu amechangia zitakwenda kuwahudumia wale wachache miongoni mwetu ambao kwa bahati mbaya watakuwa wamepata madhira ya kuugua. Kwa hivyo, kadri ambavyo tutakapoleta mapendekezo ya sheria hapa na Mungu akajalia ikapita basi tunakoelekea pengine ni pazuri zaidi kuliko tunapotoka. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa Manispaa ya Songea haina Hospitali ya Wilaya lakini pia katika Manispaa ya Songea, wakazi wengi wanategemea Kituo cha Afya cha Mji Mwema na kituo hicho hakina gari la wagonjwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta gari kwa ajili ya wagonjwa ili kurahisisha kutoa huduma pamoja na kurekebisha jengo la upasuaji ili kuweza kwenda sawasawa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali ina mkakati gani wa kuweka Kituo cha Damu Salama katika Kituo cha Afya cha Mji Mwema?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali la kwanza kuhusu ambulance, kama ambavyo tumekuwa tukisema hapa Bungeni kila siku siyo jukumu la Wizara ya Afya. Kimsingi ni jukumu la Halmashauri husika kwamba katika vituo wanavyovimiliki na wanavyoviendesha, kama kuna mahitaji ya ambulance basi Halmashauri husika iweke katika vipaumbele vyake iweze kununua ambulance hizo na kuzipeleka kwenye vituo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokifanya sisi Wizara ya Afya na naona sasa kinatuletea shida, tunaomba kwa wahisani watupe ambulance katika maeneo ya kipaumbele kama eneo la kupunguza vifo vya akinamama wajawazito na watoto, tukipata ndiyo tunatawanya kwenye Majimbo na kwenye Halmashauri kadri ambavyo tutaweza kufanya hivyo, lakini sio jukumu letu. Kwa hiyo, natoa rai kwake na kwa Halmashauri zote nchini kuweka kipaumbele cha kununua ambulace katika Halmashauri zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili linahusu damu salama. Mpaka sasa tuna upungufu wa kuwa na vituo vikubwa vya kanda vya damu salama katika mikoa saba nchini, Mikoa ya Geita pamoja na Arusha wameonesha uwezekano wa kujenga vituo vyao wenyewe. Mikoa ambayo imebaki tumeweka kwenye bajeti, mwaka jana tuliweka shilingi bilioni mbili bahati mbaya hatukufanikiwa kukamilisha, mwaka huu pia kwenye bajeti hii tumeweka tena shilingi bilioni mbili. Malengo yetu kwa kweli ni kuhakikisha mikoa hii ukiwemo Mkoa wa Ruvuma pale Songea tunajenga kituo kikubwa cha Damu Salama ili kuokoa Maisha ya Watanzania wenzetu.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa tatizo la maji la Mpanda Vijijini linalingana kabisa na tatizo la mradi wa maji wa World Bank katika kata ya Mkako, Wilayani Mbinga lakini pia katika Kata ya Litola, Wilayani Namtumbo na Kata ya Luwiko, Wilayani Songea Mjini, naomba kujua kwamba miradi hii imeonesha tayari imekamilika kwa mujibu wa taarifa, lakini haitoi maji hata kidogo, kiasi ambacho inaleta tafrani kwenye maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasanaomba nijue kwamba je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuongozana na mimi katika Mkoa wangu wa Ruvuma kwenye maeneo haya niliyoyataja ili kuona hali halisi ya miradi hiyo na kuweza kuikamilisha ili wananchi, wanawake wote wa Mkoa wa Ruvuma kwenye maeneo hayo wapate maji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kumjibu kwa haraka tu kwamba mimi nipo tayari. Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba…

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Naomba nitoe maelekezo mahsusi kwamba karibu maeneo mengi miradi hii ina matatizo. Naomba niwaagize Wakurugenzi wote wa Halmashauri zote 185 by tarehe 20 mwezi Julai tupate takwimu za miradi yote iliyokamilika ipi inatoa maji na ipi haitoi maji tuje na suluhisho la kusaidia wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, endapo tutaona kwamba, tumepata takwimu hiyo, baadaye tunaona kwamba, Mbunge analalamikia mradi fulani, lakini katika orodha haupo, tutajua kwamba, mradi ule umehujumiwa makusudi na Halmashauri husika. Kwa hiyo, hatutosita kuchukua hatua stahiki kwa watu wote ambao kwa njia moja au nyingine wameshiriki kuhujumu hii miradi, mwisho wa siku wananchi wanashindwa kupata huduma hii ya maji. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri wa Fedha, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, kwa kuwa Mkoa wa Ruvuma ni miongoni wa mikoa ambayo ni food basket nchini Tanzania, je, Serikali inachukua hatua gani za makusudi za kuweka benki hii kila mkoa badala ya kuweka benki hii kikanda? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika,swali la pili, ili kuboresha uchumi wa viwanda tunaoutarajia ambao kimsingi malighafi zinatokana na kilimo asilimia 75. Je, Serikali ipo tayari kuongeza ruzuku ya mbolea ili mbolea iuzwe Sh.10,000 kwa kila mfuko wa kilo 50 badala ya mfuko ambao unauzwa sasa Sh.60,000 mpaka Sh.65,000? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kunipa nafasi ili niweze kufafanua swali la Mheshimiwa Mbunge, Jacqueline Msongozi wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Ruvuma, hususan katika kile kipengele chake cha (b) kuhusu ruzuku katika suala zima la mbolea.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Kilimo, kama alivyosema Mheshimiwa Waziri wangu siku chache zilizopita ni kwamba tupo katika mkakati na mpango maalum katika Bunge hili la bajeti kuhakikisha kwamba ule mfumo wa ununuzi wa mbolea ya pamoja, tutawaletea semina Waheshimiwa Wabunge wote ili waweze kujua nini maana ya bei elekezi ya mbolea ili waweze kuwa na uelewa mpana nini maana ya kutoka kule kwenye ruzuku na sasa hivi tupo katika mfumo wa ununuzi wa mbolea kwa pamoja. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa asilimia 10 inayotengwa kwa ajili ya wanawake, vijana na walemavu katika Halmashauri mbalimbali katika nchi yetu zimekuwa ni jambo ambalo halijatungiwa sheria, kwa hiyo, linatoa loophole kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zetu ama kupeleka au kutopeleka.
Je, ni lini Serikali itatunga sheria au italeta marekebisho ya sheria hapa Bungeni ili jambo hili la asilimia 10 kwa makundi haya iwe ni lazima na isiwe kama vile ambavyo wanafanya Wakurugenzi kwenye maeneo mbalimbali kwamba wanafanya kwa hiari? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira kidogo kwa sababu mwezi wa sita wakati wa kupitisha Sheria ya Fedha ya mwaka 2018 kutakuwa na kipengele ambacho kitamruhusu Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa kutunga Kanuni ambazo zitawalazimisha Wakurugenzi kuhakikisha kwamba wanatenga fedha hizo asilimia 10 kama alivyopendekeza.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, inaonesha kwamba ukataji wa miti kwa ajili ya nishati ya mkaa umekuwa ni chanzo pia kikubwa sana cha kusababisha uharibifu wa mazingira. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba inaondoa VAT katika nishati ya gesi ili wananchi waweze kununua gesi hiyo kwa matumizi ya nyumbani kwa bei ndogo ili kuondokana na adha ya uharibifu wa mazingira inayosababishwa na ukataji wa miti ambalo ni tatizo kubwa katika nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa katika Ilani ya CCM, ukurasa wa 212 - 213, sehemu ndogo ya (e) tumeelekezwa na chama sisi kama Serikali kwamba lazima tuhakikishe kwamba tunaongeza kiwango cha watumiaji wa nishati mbadala kutoka asilimia 30 mpaka asilimia 50 katika kipindi cha miaka mitano. Ndiyo maana katika Wiki ya Mazingira Duniani ambapo tulikuwa na siku tano pale Dar es Salaam tuliweza kuwaalika wadau mbalimbali ambao sasa wanakuja na teknolojia ya nishati mbadala. Wananchi waliweza kwenda pale wakashuhudia namna ambavyo hizi taka ngumu zikiwemo randa za mbao pamoja na vinyesi vya mifugo, wameweza kuja na teknolojia na kubana na kutengeneza mkaa. Kwa hiyo, tunaamini kwamba tutapunguza ukataji wa miti kwa sababu ya teknolojia mbadala.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye upande wa gesi kulikuwa na ORYX wanaonyesha kutumia gesi tutatumia fedha kidogo sana ambapo huwezi kulinganisha na mkaa. Ndiyo maana Mheshimiwa Waziri wa Nishati tayari wameshahakikisha kwamba usambazaji wa gesi katika Jiji la Dar es Salaam kwa kupitia mabomba sasa umeanza. Ni lengo la Serikali kwamba tutaenda na miji mingine na miji ndiyo inayotumia mkaa zaidi kuliko vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Msongozi, naamini wewe kama mdau wa mazingira jambo hili ambalo lipo kwenye ilani tutakwenda kufanya mageuzi makubwa ya kuhakikisha kwamba tunatumia nishati mbadala badala ya kuendelea kukata miti. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Serikali ambayo kimsingi yameacha kujibu kipengele (b), sasa naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, Lusewa ni Mji Mdogo ambao sasa hivi umeshapandishwa hadhi na kuwa Mji Mdogo. Ni eneo ambalo lina wakazi wengi sana. Kutoka Lusewa kwenda Nalasi kuna umbali wa kilometa 150 na kutoka Lusewa kwenda Songea Mjini kwenye hospitali ya rufaa kuna kilometa 150. Wanawake wenzangu wa eneo hilo la Lusewa katika Mji Mdogo wamekuwa wakipata shida sana hasa kwenye suala la usalama wao wa uzazi na usalama wa mama na mtoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, wanawake na watoto wamekuwa wakipoteza maisha na siku moja nilisimama hapa katika Bunge lako Tukufu nilionesha hisia zangu kwamba imefika mahali sasa kumtoa mwanamke kwenye Kituo hiki cha Lusewa ambacho hakina theatre kumpeleka Nalasi kilometa 150, gari la kubebea hao wagonjwa hakuna, wakati mwingine ni mabovu. Naomba Serikali inipe majibu ya kina ni lini itakamilisha ujenzi wa kituo hiki cha afya pamoja na kuweka hii theatre ambayo itawasaidia akinamama hawa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, anyway siyo swali lakini ni ombi, niseme kwamba, je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuongozana nami pamoja na Mbunge wa Jimbo la Namtumbo, Mkurugenzi wa Namtumbo na DMO wa Namtumbo ili aende akaone mwenyewe kwa macho jinsi ambavyo wanawake wanavyopata tabu na watoto wanapoteza maisha katika maeneo yale? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi kwamba ujenzi wa kituo kile cha afya umekamilika isipokuwa chumba cha upasuaji kilichobaki ni sakafu peke yake. Naomba nitumie fursa hii kumuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ahakikishe kwamba katika vyanzo vyake vya mapato kwa kushirikiana na wananchi kazi ya kumalizia sakafu iweze kukamilika ili wananchi waendelee kupata huduma badala ya kusubiri mpaka hicho kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020. Naamini kabisa katika vyanzo vyao vya mapato wakijibana wanaweza kumalizia kabisa suala zima la sakafu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameomba mimi kuambatana na Waheshimiwa Wabunge wa maeneo hayo. Naomba nimhakikishie, katika maeneo ambayo nina deni la kwenda kujionea mimi mwenyewe ni pamoja na Mkoa wa Mtwara lakini nikitoka Mtwara nitakuwa naenda Ruvuma halafu nitakwenda Njombe. Ilikuwa niende kwa bahati mbaya nikawa nimepatwa na msiba. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira. (Makofi)
MHE. JACQULINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitishwa sana na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jambo kubwa hili la Mawakala wa Pembejeo. Pamoja na majibu hayo, naomba niulize swali moja dogo la nyongeza lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
• Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokuwalipa Mawakala kwa wakati kwa kisingizio cha uhakiki kwa kipindi cha miaka minne ambapo Mawakala hao wamekuwa wakiishi kwa shida, wamekuwa wakifilisiwa mali zao na wengine wamekuwa wakipoteza maisha, naomba sasa commitment ya Serikali, ni lini Serikali itawalipa mawakala hao?
• Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inachelewesha malipo ya mawakala kwa zaidi ya miaka mitatu na thamani ya fedha kwa huduma waliyotoa haitalingana na thamani hiyo endapo wangelipwa kwa wakati. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwalipa mawakala hawa fedha zao ikiwa ni pamoja na riba ya asilimia tano?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninaelewa concern ya Mheshimiwa Mbunge, ninaamini pia na Wabunge wengi na hata katika bajeti yetu ya Wizara ya Kilimo alitoa na machozi, nampa pole katika hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi kabisa ni kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ina nia njema na intention yake siyo kwamba haitaki kuwalipa mawakala hawa wa pembejeo, lakini kwenye jibu langu la msingi kama nilivyosema ni kwamba uhakiki unaendelea na uhakiki huu ni wa kina; na mara utakapofanyika sisi kama Serikali tutatoa taarifa na vilevile kama Wizara ya Kilimo wale wahusika wote ambao walikuwa chini yetu watumishi wa Serikali, tumeshawafukuza kazi.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, ile bakora ulioitumia wewe kumchapia yule jamaa nadhani ilikuwa ni bakora maalum sana. Sasa nilikuwa nataka niulize swali kwamba ni aina gani ya material yatakayotumika kutengeneza hicho kiboko cha kuchapia wanafunzi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, kanuni hazielezi kuhusu ni material gani itumiwe kutengeneza fimbo, lakini wanasema iwe ni fimbo ambayo haijakakamaa ambayo ni laini.

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kusisitiza kwamba, tunaporuhusu viboko haturuhusu uchapaji ambao una madhara kwa mwanafunzi. Kwa hiyo hata kama unatumia kiboko tumia kile ambacho hakina madhara na kwa njia ambayo haidhuru. Vilevile sheria imeelekeza kwamba unachapa wapi, wanasema unachapa mkono au kwenye unachapa kwenye makalio, sio kichwa au mgongo. Kwa hiyo, sheria ile ikifuatwa vizuri, kanuni zile zikifuatwa, tusingekuwa tunapata madhara ambayo tunapata kwa sasa hivi.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza pia Mbunge wa Jimbo la Peramiho, dada yangu, Mheshimiwa Jenista Mhagama, kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia ujenzi wa barabara hii na hata alipokuja Mheshimiwa Rais, alijaribu kusema pale ili barabara hii iweze kujengwa.

(a) Swali langu la kwanza; ni kwa nini Serikali inachukua muda mrefu sana kufanya upembuzi yakinifu lakini pia na usanifu wa kina? Barabara hii imechukua karibu miaka kumi kupitia maneno hayo ya upembuzi na usanifu. Ni lini Serikali itamaliza upembuzi huu na usanifu huu ili barabara hii ianze kujengwa?

(b) Swali la pili; licha ya Serikali kuonesha kwamba imetenga shilingi bilioni 5.86, lakini fedha hizi hazikuweza kwenda kwa mwaka 2018/2019: Je, Serikali haioni kwamba kutokupeleka fedha hizi inaendelea kuchelewesha maendeleo kupitia barabara hii kwa wananchi wa Mkoa wa Ruvuma, hususan Jimbo la Peramiho?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, uniruhusu tu nimpongeze Mheshimiwa Jacqueline, lakini nimpongeze Mbunge wa Peramiho kwa kufuatilia kwa sababu amekuwa akifuatilia sana jambo hili. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge mwuliza swali kwamba inachukua muda mrefu kwa sababu kwanza mtandao wa barabara ni mkubwa, mahitaji ya ujenzi ni makubwa na tunaendelea kutafuta fedha na kutenga fedha. Hata mwaka unaokuja tutaliomba Bunge lako liweke fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawasiliana na wenzetu wa Wizara ya Fedha. Tukipata fedha tu mara moja tutatangaza na kuanza kujenga barabara hii. Kwa hiyo, kwa majibu hayo, Mheshimiwa Jacqueline avute subira kidogo, tumejipanga vizuri, mahitaji ni makubwa, tunakuja Peramiho kuhakikisha kwamba tumewaunga wananchi wa…

MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa Kemi.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja dogo la nyongeza lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii katika suala la usanifu na upembuzi wakina sasa hivi limechukua miaka nane. Sasa swali langu ni kwa nini Serikali inachukua muda mrefu kiasi hiki kwa ajili ya kufanya tu usanifu na upembuzi wa kina?

(b) Barabara hii imebeba uzito mkubwa sana katika kuharakisha shughuli za kiuchumi ili tuweze kufikia uchumi wa kati itakapofika mwaka 2025. Lakini kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri kwamba upembuzi yakinifu unaendelea na usanifu mpaka inakapofika Juni, 2020 ninapata mashaka kwamba huenda hii barabara ikaendelea kuchelewa ziadi.

Je, Serikali haioni kwamba kutoleta maendeleo au kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami ambayo inapita katika kata zifuatazo zinazoendelea kujishughulikisha katika shughuli za uchumi ikiwa pamoja na makaa ya mawe yanayochimbwa huko? Lakini pia shamba kubwa la miwa linaloenda kuanzishwa huko. Na kata hizo ningependa nizitaje, ni kata ya Likuyufusi, Litapwasi, Ndogosi, Muhukulu lilayi na Muhukulu barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini sasa serikali itakwenda kuanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza uniruhusu nitumie nafasi hii nishukuru kwa swali nzuri lakini niseme tu, eneo hili la Likuyufusi barabara hii ya Likuyufusi Mkenda ni barabara ambayo inagusa majimbo mawili; Jimbo la Peramiho kwa Mheshimiwa Jenista Mhagama, lakini pia inawahudumia kwa kiasi kikubwa wananchi wa jimbo la Nyasa. Ambapo kuna kazi kubwa imefanyika kwa sababu barabara hii ina wapunguzia adha wananchi wa kata hii ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwa juhudi ambazo zinafanyika na kwa ushirikiano mkubwa kwa Mheshimiwa Jacqueline na Wabunge wa majimbo inayofanyika, barabara hii ipo katika ubora kwa kuzingatia mahitaji ambayo nimeyata. Tunatambua kwamba ili tuweze kujenga uchumi ni lazima miundombinu iwe bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetembelea na nimejionea namna ambavyo Waheshimiwa Wabunge hawa akinamama, na niseme Wabunge wakinamama kazi nzuri wanafanya. Nimekwenda kule nimeona kule Mitomoni kuna MV Stella inasaidia wananchi wale kuvuka ili watumie barabara hii ambayo kwa kiasi kikubwa tumeiboresha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumejipanga vizuri. Wakati harakati za kujenga barabara ya lami zinafanyika, tunazingatia kwa kiasi kikubwa kuhakikisha barabara hii inakuwa bora. Yako maeneo ambayo tumeweka madaraja ya chuma, yako maeneo tumeelekeza ili wakati huu tunafanya harakati za kuhuisha kujua gharama halisi za ujenzi wa barabara za lami, barabara hii inakuwa bora na makaa ya mawe yanabebwa, hata mwekezaji anaendelea na harakati zake za uwekezaji wa kiwanda cha sukari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumejipanga vizuri, tutawa-support wananchi wa maeneo haya ya Peramiho, wananchi wa Kata alizozitaja ili nao waende katika harakati; hatupendi tukifika uchumi wa kati wawe chini ya mstari ule wa wastani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, tumejipanga vizuri kwenda kuiboresha barabara hii. Waheshimiwa Wabunge wa maeneo hayo; Mheshimiwa Mhagama na Mheshimiwa Manyanya, tumejipanga vizuri, vuteni subira, muwe comfortable, tutaenda kuijenga barabara hii muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekwenda Mkenda nimeona pia kuna soko zuri, nimeona wananchi wa kule Msumbiji wana mahitaji makubwa ya mahindi ambayo yanazalishwa upande wa Peramiho. Kwa hiyo, tunatambua umuhimu huo wa kufanya maboresho ili wananchi hawa waweze kupata manufaa makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza maswali ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Eng. Makani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, nimpongeze Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana na Naibu wake kwa utendaji mzuri wa kazi. Pamoja na majibu hayo naomba maswali madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ni lini Serikali itashughulikia changamoto katika kaya za vijiji kwenye Tarafa za Nakapanya, Matemanga, Nampungu na Mlingoti? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni lini Serikali itapitia upya utaratibu wake na kuhakikisha kwamba wanufaika wanakuwa ni wale wenye kaya maskini na siyo wale wenye uwezo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa
Mwenyekiti, naomba nimjibu maswali madogo mawili ya nyongeza wifi yangu Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kama mwanamke naomba nimpongeze kwa sababu walengwa wengi ambao ni wanufaika wa kaya maskini ni wanawake kwa sababu wameonyesha uaminifu mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika swali kuhusu Tarafa za Napakanya, Matemanga, Nampungu na Mlingoti, naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi TASAF tumekuwa katika Awamu ya Tatu na mwezi ujao Oktoba tunategemea kuzindua rasmi sehemu ile ya pili ambapo tumemaliza sehemu ya kwanza. Hizi Tarafa zote nne ambazo amezisema basi walengwa wote wale ambao hawajafikiwa watafikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili, naomba niseme kwamba Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Mpango huu wa Kunusuru Kaya Maskini tumejipanga kuboresha zaidi kuhakikisha kwamba walengwa wote ambao tulikuwa tunawawezesha na sasa hivi wameweza kusimama wenyewe, tutakuwa na mpango mkakati kuhakikisha kwamba wamefuzu tunaita graduation ili sasa waweze ku- phaseout ili tuweze kusaidia wale wengine ambao hawajiwezi kwa sababu wasiojiweza, maskini sana, wazee, walemavu wapo kila siku basi tuendelee kuwahudumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, tumeboresha mfumo kuhakikisha kwamba kuanzia sasa hivi tutakwenda kielektroniki ili kuondokana na suala zima la kaya hewa. Niwatake Wabunge wote na Watanzania wote kuhakikisha kwamba wanaendelea kuunga mkono juhudi hizi za Serikali ya Awamu ya Tano kuhakikisha kwamba walengwa wote wanaotokana na kaya maskini ndiyo hao wanaostahili kupewa misaada yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili name niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika sana kwa majibu ya Serikali namna yalivyo. Ilikuwa tarehe 7 Februari, 2018 kwenye swali langu namba 93, niliuliza swali kuhusiana na kiwanda hiki hiki cha SONAMCU, majibu ya Serikali niliambiwa kwamba ikifika mwezi wa nane mwaka jana, kiwanda hiki kitakuwa kimeanza kufanya kazi, lakini mpaka leo hii ni takribani mwaka mmoja na miezi minne, kiwanda hakijaanza kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niulize swali moja dogo la nyongeza, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Ni kwa nini Serikali inawadanganya wananchi wa Mkoa wa Ruvuma hususan Songea na Namtumbo?

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kutokufanya kazi kwa kiwanda hiki, Serikali haioni kama inapoteza ajira kwa wananchi 2500, lakini pia Serikali haioni kama inakosesha Serikali mapato? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika,naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kadri ambavyo nitachagua kama ifuatavyo, kwa sababu nimeulizwa mengi kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimfahamishe Mheshimiwa Msongozi, uwekezaji katika kiwanda hicho unafanywa na sekta binafsi. Wajibu wa Serikali ni kuwezesha na kazi ambayo imefanyika. Kuhusiana na mazingira yaliyoko sasa, kwanza kabisa mwekezaji alikuwa anadai VAT Refund na wakati huo huo kabla ya kulipwa anastahili kuchunguzwa hapo ambapo itaonekana alichodai ndicho kiachostahili atarejeshewa na ndipo atakapowezeshwa sasa kuendelea na shughuli zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo hatuna nia ya kuwakatisha tamaa wananchi wa Songea wala Namtumbo. Kwa hiyo, kwa misingi hiyo, kiwanda hiki kitaendelea kuhamasishwa na kuwezeshwa ili kuweza kufikia malengo ambayo yamekusudiwa. Niwaombe sana wananchi wa Mkoa wa Ruvuma ambao mimi pia ni mwananchi wa Mkoa wa Ruvuma, tunayo dhamira ya dhati ya kuona kwamba, ajira zilizokuwa zinapatikana kupitia kiwanda hiki zinarejea na wananchi wananufaika.
MHE. JACQEULINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwa niaba ya Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum Rukwa, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Rukwa ni mkoa wenye vivutio vya utalii, lakini pia Mkoa wa Rukwa unajishughulisha na masuala ya uvuvi katika Ziwa Tanganyika. Mkoa wa Rukwa ni mkoa ambao umeshika nafasi ya tatu kitaifa katika uzalishaji wa mazao ya nafaka. Pamoja na hivyo Serikali bado haijajenga uwanja huo. Swali la kwanza, je, Serikali haioni kama ucheleweshaji wa ujenzi wa uwanja huu unasababisha udumavu wa ukuaji kiuchumi wa Mkoa wa Rukwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wananchi wa Mkoa wa Rukwa wamekaa muda mrefu sana hawajapata uwanja wa ndege; je, ni lini Serikali itaanza kujenga uwanja wa ndege wa Mkoa wa Rukwa ili kuwafanya wananchi wa Mkoa wa Rukwa wanufaike na matunda mazuri ya Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia kuhakikisha kwamba uwanja huu unajengwa. Katika swali la kwanza la nyongeza ameeleza kwamba kuna vivutio vya utalii tunakubali uvuvi, lakini pia ni kati ya mkoa unaozalisha. Serikali tayari imeshapata fedha, sasa hivi kilichopo tu ni kuanza ujenzi. Kwa hiyo, kwa sababu hiyo Serikali imelitambua hili, hivyo, hakutakuwa na sababu ya kuwa na udumavu kwa sababu tayari uwanja huo utaanza haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini Serikali itaanza kujenga uwanja huo? Katika jibu langu la msingi nimesema kila kitu kimeshakamilika, ni taratibu tu za mwisho za kibenki ambazo lazima zifanyike ili uwanja huo uanze. Kama mkandarasi tayari ameshapatikana kwa hiyo, tuna hakika ujenzi utaanza mara moja. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Jenista Joachim Mhagama kwa namna ambavyo halali usiku na mchana anafuatilia kuona kwamba barabara hii inajengwa ili kuweza kuchochea uchumi wa wananchi wa maeneo husika Mkoa wa Ruvuma na Nchi yetu ya Tanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wetu wa Ruvuma ni mkoa ambao umeshika nafasi ya kwanza mara tano mfululizo kwa uzalishaji wa mazao ya nafaka. Wananchi wa maeneo hayo wanajishughulisha na kilimo, uzalishaji wa makaa ya mawe, soko la mazao la Kimataifa, lakini pia kuna shamba la miwa.

Mheshimiwa Naibu Spika…

NAIBU SPIKA: Naomba uulize swali Mheshimiwa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najenga hoja. Swali la kwanza, je, Serikali haioni kuwa kuchelewesha ujenzi wa barabara hii ni kuendelea kufanya udumavu wa maendeleo kwenye maeneo husika hasa kwa Mkoa wa Ruvuma na Jimbo la Peramiho na kwa nchi yetu kwa ujumla? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nafahamu kwamba Kamati ya Bajeti imetenga fedha shilingi milioni 110 kwa ajili ya kufanya usanifu wa ujenzi wa daraja, daraja ambalo limekwishajengwa, daraja la Mkenda. Je, ni kwa nini Serikali sasa isihamishe fedha hii shilingi milioni 110 ikaanze ujenzi wa barabara mara moja ili kuweza kuchochea uchumi wa maeneo husika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii na kwa kutambua umuhimu wa uzalishaji ambao uko katika Mkoa wa Ruvuma lakini pia na makaa ya mawe; katika jibu langu la msingi tumesema barabara hiyo pia ni muhimu sana kwa ulinzi wa nchi yetu na pia ni moja ya vipaumbele vya nchi kuunganisha nchi na nchi na hii ni trunk road wala sio regional road. Ndiyo maana tayari barabara hii imeanza kutengewa fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kama Mheshimiwa Mbunge amenisikiliza vizuri, kulifanyika usanifu wa awali ambao wakati huo barabara haikuwa na matumizi ambayo inayo sasa hivi na ndiyo maana kukafanyika redesign yaani usanifu mpya kwa sababu tayari sasa kule kuna makaa ya mawe na mgari yaliyokuwa yanapita wakati ule wakati barabara inafanyiwa usanifu siyo ambayo sasa yanapitika. Kwa hiyo lazima lile daraja lifanyiwe usanifu mpya ili liweze kumudu shughuli ambazo sasa zitaweza kufanyika kwa maana ya kuwa na uwezo wa kuhimili magari ambayo yatapita na uzito wake hasa baada ya kugundua makaa ya mawe na kuongezeka kwa traffic kwenye hiyo njia. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja la nyongeza, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Tunduru, na kwa Kata hizi zilizotajwa; Tinginya, Malumba, Kalulu, Mindu, Narasi Mashariki na Narasi Magharibi, ni kata ambazo hazina vituo vya afya. Lakini pia zinazungukwa na Selous Game Reserve. Wakati mwingine unakuta wale akinamama wanaokwenda kujifungua, haja ya kujifungua inawapata wakati wa usiku ambapo sasa kutoka maeneo waliyopo mpaka kufika kwenye hospitali ya wilaya pana zaidi ya takribani kilometa 80 mpaka 100 na wakati mwingine sasa wamekuwa wakipata majanga ya kuvamiwa na tembo, wanyama wakali kama simba na chui.

SPIKA: Swali.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ni lini sasa Serikali itaona umuhimu wa wananchi hawa kujengewa vituo vya afya ili waweze kuondokana na adha hiyo?

(b) Mheshimiwa Spika, maeneo hayo yote niliyoyataja yana zahanati tu, na zahanati zao wakati mwingine unakuta hazina watumishi wa kutosha. Zahanati moja ina mtumishi mmoja na kwamba akiumwa huyo mtumishi ni wiki nzima hakuna huduma ya afya. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba zahanati hizo zinapelekewa wahudumu wa afya ili waweze kupata huduma inayostahili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ameuliza kwamba lini Serikali itaona umuhimu wa kujenga vituo vya afya katika maeneo hayo. Na nilishalijibu katika jibu langu la msingi kwamba kwa kadri ya upatikanaji wa fedha Serikali tutaendelea kujenga katika maeneo husika, na nimhakikishie kabisa kwamba Serikali inazingatia umuhimu wa maeneo hayo ambayo wananchi wanatokea. Kwasababu kama alivyoeleza hapo awali kwamba kuna changamoto nyingi. Kwa hiyo, nimhakikishie tu kwamba tutayaingiza katika mpango na fedha itakavyopatikana ataona matokeo yake.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ameeleza kwamba katika maeneo hayo watumishi/wahudumu wa afya hawapo wa kutosha. Na sisi kama Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya tuna huo mpango, kwa kadri tunavyokuwa tunaajiri kutokana na vibali ambavyo tunapatiwa tutaendelea kuwatenga. Kwa hiyo, hata maeneo hayo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutaendelea kupeleka kulingana na vibali vya ajira ambavyo serikali itakuwa inatupatia. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali iliona umuhimu wa kujenga barabara hii na barabara hii ni ya kimkakati dhidi ya masuala ya kiuchumi ambayo inakwenda kujengwa kwa ajili ya kuinua uchumi wa Kikanda, Kimkoa na Kitaifa, na barabara hii ilishafanyiwa upembuzi wa kina na upembuzi huo ulishakamilika toka mwaka 2018. Je, ni lini Serikali itatoa fedha kupeleka huko kwa ajili ya kuana ujenzi huo haraka iwezekanavyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ucheleweshaji wa ujenzi wa barabara hii ya kimkakati ambao unachukua muda mrefu sana kuanza kujengwa je, Serikali haioni kwamba kutokuanza kujenga barabara hii kwa haraka inaendelea kusababisha udumavu wa ukuaji wa uchumi katika Mkoa wa Ruvuma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ina urefu wa kilometa 521 kwa hiyo ni uwekezaji mkubwa na tayari tulishaanza jitihada za kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami kwa hatua za awali ikiwa ni pamoja na hizo hatua ambazo tayari zimeshafanyika usanifu wa kina lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Msongozi kwamba tayari tumeshaanza ujenzi wa kiwango cha lami katika vipande kadhaa ambavyo nimevitaja ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kiwango cha lami kilometa 66.9 kuanzia Kidatu kwenda Ifakara, na bado tumehakikisha kwamba barabara hii itakwenda kutengenezwa kadri fedha zitakapokamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nia ya Serikali ni kuikamilisha barabara hii ili kuifungua Ruvuma na kanda yote ya kusini ambayo inatumia barabara hii. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kadri fedha zitakapoendelea kupatikana barabara hii tutahakikisha tunaiunganisha kwa Mikoa ya Ruvuma na Morogoro kupitia kwenye hiyo barabara ambayo amesema ambayo inapita kwenye mbuga za Selous na ni miinuko mikali kwa hiyo, uwekezaji ni mkubwa lakini Serikali inatafuta fedha na tunahakikisha tutaijenga, ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ili niweze kuuliza swali moja dogo la nyongeza lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri, lakini asilimia zinatotajwa hapa za mgao wa dawa unaokwenda katika Kituo cha Afya hiki si sawa na uhalisia uliopo kwenye eneo la tukio.

Mimi nimuombe sasa Naibu Waziri baada ya Bunge hili aje katika kituo hicho cha afya ajionee uhalisia wa mgao huo wa dawa kwa sababu wananchi bado wanahangaika. (Makofi)

(b) Mheshimiwa Spika, katika kituo hicho cha afya wananchi wamejitolea kujenga jengo la upasuaji kwa gharama zao wao wenyewe na kwamba wamekwama katika masuala ya vifaa vya madukani; bati, boriti, nondo, rangi na mambo mengine yanayohusiana na vifaa vya dukani. Kwa misingi hiyo, je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia katika kituo hiki cha afya ili kuweza kuwawezesha wananchi hawa waweze kupata Kituo cha Afya na nguvu zao zisipotee bure? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana; naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu katika swali la msingi kwamba Serikali imeweka utaratibu uko wazi kwamba zahanati inapopandishwa hadhi kuwa Kituo cha Afya maombi ya Halmashauri husika yanapelekwa kwa Katibu Mkuu Afya ili kupata mgao wa dawa kwa ngazi ya kituo cha afya na si zahanati kama ilivyokuwa mwanzo.

Kwa hiyo, naomba kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Jacqueline Msongozi Ngonyani kwa kazi kubwa anayofanya kufuatilia huduma za afya katika kituo hiki cha afya, lakini nimhakikishie kwamba tumeshaelekeza Halmashauri ilete maombi hayo na tutahakikisha sasa mgao wa dawa unaendana na kituo cha afya ili wananchi wasipate changamoto ya upungufu wa baadhi ya dawa.

Mheshimiwa Spika, pili nipongeze sana wananchi wa Namtumbo na katika eneo hili la Msindo kwa kuchangia maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Afya na kuanza ujenzi wa jengo la mama na mtoto, lakini pia jengo la upasuaji. Nimhakikishie kwamba tutahakikisha na sisi kama Serikali tunakwenda kufanya tathmini na kutafuta fedha kuunga mkono nguvu za wananchi ili Kituo cha Afya kiweze kufanya kazi vizuri zaidi, ahsante sana.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona nipende kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo. Barabara ya Likuyufusi Mkenda ina urefu wa kilometa 124 na ni barabara ya kimkakati inayounganisha Mkoa wa Ruvuma na nchi yetu ya Mozambique.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Ngonyani kama ifuatavyo. Ni kweli barabara hii Mheshimiwa Jenista amekuwa akiuliza muda mrefu ni barabara muhimu tunaijua na ina maendeleo makubwa kwa ajilii ya wananchi wa kule kwa vile Mheshimiwa Ngonyani naomba nikwambie kwamba hii barabara tunaitambua vizuri na iko kwenye mpango wa Serikali na sasa tuko kwenye hatua za mwisho za kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo.
MHE. JACQUELINE N. MAONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Sasa naomba niulize swali la nyongeza, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, mpaka sasa hivi Serikali bado haijawa na majibu sahihi kwa wakati sahihi yanayohusiana na suala la mbolea, ambayo kimsimgi imepanda bei katika maeneo yote ya nchi yetu ya Tanzania, hususan Mkoa wa Ruvuma: Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka ruzuku kwenye mbolea ili wananchi waweze kupata mbolea kwa bei nafuu?

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, Mkoa wa Ruvuma ndiyo benki ya chakula nchini Tanzania; na bila shaka yoyote Mkoa wa Ruvuma umeongoza takribani miaka minne mfululizo kwa uzalishaji wa mazao ya nafaka: Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kiwanda cha uzalishaji wa mbolea katika nyanda za juu Kusini, hususan Mkoa wa Ruvuma ikiwa ni pamoja na kuweka benki ya kilimo katika Mkoa wa Ruvuma? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hakuna njia ya mkato kwenye sekta ya kilimo zaidi ya ku-design modal ya kutoa ruzuku. Nataka nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba, ilikuwa ni vigumu kwa mwaka huu kutengeneza mfumo wa ruzuku kwenye bei ya mbolea kwa sababu, historia inaonesha mifumo ya awali iliharibu na mifumo ile ilisababisha fedha nyingi za umma kupotea na wakulima hawaku-benefit na mfumo wa ruzuku uliokuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilihakikishie Bunge lako Tukufu, maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kwamba, Wizara ya Kilimo tutengeneze mechanism ambayo itatuletea mfumo sahihi wa ruzuku kwa pembejeo. Tutaleta mfumo wa stabilization fund na katika bajeti ya mwaka kesho mtaiona na tutaiwekea mkakati ili ruzuku iweze kwenda moja kwa moja kuwafaidisha wakulima. Hiyo ndiyo njia pekee itakayoweza kuwalinda wakulima wetu wadogo na huo ndiyo mwelekeo wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba tungetoa ruzuku leo, tusingekuwa na framework ambayo ingeweza kumfaidisha mkulima, bali kwenda kupoteza fedha za umma na hiyo isingekuwa haki kwa nchi. Kwa hiyo, kuanzia mwaka ujao wa fedha 2022/2023 tunaleta mfumo wa Stabilization Fund itakayotumika kwenye pembejeo na pale ambapo mazao ya wakulima yanaanguka kwa sababu zilizo nje ya uwezo wetu, ili kuwalinda wakulima wetu wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kujenga kiwanda; uwekezaji wa kiwanda unaangalia variables nyingi sana, siyo tu kwa sababu eneo fulani linazalisha mazao mengi, upatikanaji wa rasilimali kwa maana ya raw materials na zipo sababu nyingine. Siwezi kutoa ahadi ndani ya Bunge lako kwamba Serikali itaenda kujenga kiwanda katika Mkoa wa Ruvuma, lakini kama atatokea mwekezaji anataka kujenga kiwanda Mkoa wa Ruvuma, sisi kama Serikali tutamsaidia na kum-support ili aweze kujenga. Tunachokifanya, tunamsaidia mwekezaji wa intracom aliyeko hapa Dodoma ili aweze kuzalisha mbolea kutokana na ikolojia ya nchi yetu na yasitokee makosa yaliyotokea huko nyuma kwenye kiwanda cha Minjingu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mambo ambayo tunayafanya na tunawapa support. Kwa hiyo, kuna kiwanda hiki cha hapa Dodoma; na vilevile tumewasaidia Minjingu kwa ajili ya kupata fedha waweze ku-expand kiwanda chao cha Minjingu ili kiweze kufikia zaidi ya tani 100,000 tuweze kukidhi mahitaji ya nchi. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza kabisa nimpongeze sana Naibu Waziri kwa namna anavyojibu maswali kwa umakini na umahiri mkubwa. Ingawaje leo ni siku yake ya kwanza, Mungu ambariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali, je, Serikali imejipangaje kuongeza ndege nyingine ili kuweza kukidhi ushindani wa soko la ndani ya nchi na nje ya nchi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Ruvuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye majibu ya awali kwamba Serikali imenunua ndege 11 na sasa imejipanga kununua ndege zingine tano, ambazo zitagharimu trilioni 1.7. Nimpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa hizi fedha na hizi ndege zitaingia ndani ya nchi mwaka 2022. Kwa hiyo tutaendelea kuboresha shirika letu la ndege nchini na ndege hizo ni ndege zile kubwa kwa maana ya moja aina ya boeing Dreamliner aina ya 787-8 ambayo ina uwezo wa kubeba abiria 262. Pia ndege zingine mbili aina ya Airbus A220-300 zenye uwezo wa kubeba abiria 181 na ndege ya mizigo yenye kuweza kubeba tani 51 pamoja na ndege aina ya Dash 8400 aina ya Bombadier ambayo ina uwezo wa kubeba abiria 76. Kwa hiyo, kutoka zile 11 za awali jumlisha tano ambazo tutanunua na Serikali tayari imesha-approve bajeti zitakuwa ndege 16 jumlisha na ndege moja iliyokuwepo awali kabda ya hizi ndege 11 zitakuwa ndege jumla 17. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Morogoro.

Je, ni lini Serikali itahakikisha dawa zote zinazohitajika kwenye wodi za kinamama na vipimo vyote zinapatikana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Kituo cha Afya cha Mkoani Ruvuma, Wilaya ya Songea, Kata ya Ruvuma, kumekuwa na tatizo la Madaktari na Matabibu ambao ni wachache sana hawakidhi kutoa huduma ya afya ipasavyo.

Je, ni lini Serikali itaongeza Madaktari na Matabibu kwenye kituo cha afya hiki ili huduma sahihi ziendelee kutolewa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, tumeendelea kuboresha upatikanaji wa dawa lakini pia vitendanishi na vifaa tiba katika vituo vyetu. Katika kipindi cha mwaka huu fedha nyingi zimetengwa kwa ajili ya kununua vifaa tiba, Bilioni 69.95 kwa ajili ya kununua vifaatiba katika Vituo vya Afya 530 nchini kote.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha uliopita, bajeti ya dawa imeongezeka na mwaka huu wa fedha bajeti ya dawa imeongezeka. Kwa hiyo, nimhakiksishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imedhamiria kuhakikisha inaondoa changamoto ya upungufu wa baadhi ya dawa kwenye Wodi za Wazazi lakini kwenye vituo kwa ujumla lakini kuboresha huduma za vipimo vya maabara.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na Kituo cha Afya katika Kata ya Ruvuma juu ya uchache wa Madaktari na Matabibu, Serikali imeendelea kuajiri watumishi, mtakumbuka mwisho mwa mwaka uliopita watumishi wa afya zaidi ya 7,000 wameajiriwa na kupelekwa nchini kote, zoezi hili ni endelevu tutaendelea kuajiri kwa kadri ya upatikanaji wa fedha ili watumishi hawa watoe huduma bora za afya katika vituo.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Barabara ya kilometa zaidi ya 300 ambayo inatoka Lumecha Kupitia Msindo – Mputa – Kitanda mpaka Londo kwa Mpepo Morogoro, imefanyiwa Upembuzi na usanifu wa kina kwa muda mrefu sana.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kwa haraka sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya inayoanzia Lumecha- Kilosa kwa Mpepo, Malinyi hadi Ifakara kama alivyoisema, tumejibu mara kwa mara kwamba imeingizwa kwenye mpango wa EPC+F, na hivi tunavyoongea wakandarasi wameshaoneshwa hizo barabara na wako wanaandaa zabuni kwa ajili ya kuijenga kwa mfumo huo wa EPC+F, ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza lenye sehemu (a) na (b) kama ifutavyo: -

(a) Je, Mhesnimiwa Naibu Waziri, anaweza kunieleza ni vikundi vingapi na kwa kiasi gani vya wanawake wa Mkoa wa Ruvuma wamekopeshwa fedha hizo?

(b) Serikali ina mpango gani wa kutumia survey data ili kuwa ni dhamana ya kuweza kuwakopesha hao wachimbaji wadogo wadogo kwa sababu wachimbaji wengi hawana dhamana ya kuweka kwenye mikopo yao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili madogo au swali moja lenye kipengele (a) na (b) la Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Ruvuma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa idadi ya waliokopeshwa kutoka Mkoa wake, hatujaweka mchanganuo wa kimkoa lakini kwa ujumla wakiweko wachimbaji wadogo wanawake na wanaume hadi sasa zaidi ya vikundi na wachimbaji wadogo 110 wameshafikiwa na mikopo kutoka mabenki ya ndani ambayo yamekubali kukopesha wachimbaji waliokidhi vigezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa swali lake la pili kuhusu data za jiolojia kutumika kama dhamana ya kupata mikopo ya benki, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi ni kwamba, tutakapokuwa tumepata hivi vifaa vya kuwasaidia wachimbaji wadogo kwenye utafiti, data zile sasa zitatumika kama mojawapo ya vigezo ikiwepo pia wao kuweka kumbukumbu za uchimbaji wao, ndiyo maana hata waliofanikiwa kufanya hivyo hadi sasa, watu 110 walio kwenye mnyororo wa thamani wa madini wameshakopeshwa zaidi ya Bilioni 80 na Benki ya NMB na Benki ya CRDB pia imeshawakopesha kiasi cha Bilioni 65. Kwa hiyo, Bilioni 145 zimeshawasaidia wachimbaji waliojipanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa wito kwa wanavikundi walioko katika Mkoa wake nao wajipange, waweke taarifa zao sahihi na mitambo hii ikija tutafanya utafiti na wataweza kutumia kama moja ya vigezo. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa hii fursa.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua ni lini Serikali itajenga barabara ya kimkakati kwa kiwango cha lami yenye urefu wa Kilomita 176 inayotoka Kitahi, kupita Amani - Makolo, Paradiso, Rwanda, Lituhi, Mbaha, Lundo, mpaka Mbamba Bay kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jacqueline Msongozi Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ambayo inaanza Kitahi, kupitia Amani – Makolo, Rwanda hadi Lituhi ipo kwenye utangazaji kwa ajili ya kuijenga barabara yote. Kuanzia Kitahi kwenda Mbamba Bay usanifu umeshakamilika na Serikali inatafuta fedha kuijenga barabara hiyo ambayo pia ni sehemu ya barabara ya ulinzi hadi Mtwara. Ahsante.(Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa nini Serikali inadhoofisha ustawi wa Ziwa Nyasa katika Mkoa wa Ruvuma ikiwa pamoja na kuwadhoofisha wananchi wa Mkoa wa Ruvuma hususani Wilaya ya Nyasa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Rais ametenga shilingi bilioni 20 kwa ajili ya kuendeleza Maziwa, lakini bilioni 20 hizi zote zinapelekwa katika Ziwa Victoria, je, kwa nini Serikali haiweki uwiano sahihi katika Maziwa yote haya matatu ikiwemo Ziwa Victoria, Ziwa Nyasa na Ziwa Tanganyika? (Makofi)
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa fursa hii ya kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jacqueline Msongozi.

Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu swali hili kwa ruhusa yako sekunde moja, naomba nitumie fursa hii ndani ya Bunge hili Tukufu, kumshukuru Mwenyezi Mungu na pili kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani yake kwangu na kunikabidhi kazi hii ya kuongoza Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Naomba pia niendelee pia kuomba ushirikiano kwa Waheshimiwa Wabunge wenzangu wakati wote wa kutekeleza majukumu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maswali ya Mheshimiwa Msongozi la kwanza juu ya kudhohofisha Ziwa. Nataka nimhakikishie yakwamba Serikali haina mpango wa kudhoofisha Ziwa Nyasa na katika bajeti hii ya 2022/2023 na hata katika bajeti ya 2021/2022 Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inayo mambo iliyofanya katika Ziwa Nyasa ikiwemo ujenzi wa Soko katika Jimbo la Nyasa linaloongozwa na Mheshimiwa Mbunge Engineer Stella Manyanya. Hivi sasa tupo katika hatua ya mwisho ya kukamilisha hatua za ujenzi wa soko lile ilimradi tuweze kuliruhusu liweze kutumika, lakini kama haitoshi kuhusiana na…

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, tusaidie kufupisha hayo majibu tafadhali.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jibu la pili, uwiano, katika jibu la msingi alilolitoa Mheshimiwa Naibu Waziri ambaye nampongeza kwa majibu yale mazuri, ni kwamba hatua ya mwaka huu ni hatua ya Ziwa Nyasa. Naomba Mheshimiwa Mbunge Msongozi na Wabunge wa Mkoa wa Ruvuma, lakini pia vilevile na Wabunge wa Mkoa wa Kigoma wawe na uhakika kwamba sasa zamu yao na wao inafikiwa baada ya hatua hizi za msingi kuwa zimetekelezwa ikiwa ni pamoja na Ziwa Rukwa pia vilevile litafikiwa, ahsante sana. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri sana ya Serikali, pamoja na hivyo bado naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Sera ya Taifa inaeleza kwamba maeneo ya pembezoni mwa Miji na Manispaa yatakwenda kuwekewa umeme kwa gharama ya shilingi 27,000 na siyo shilingi 300,000 kama ilivyo sasa.

Je, ni kwanini Serikali inakwenda kinyume na sera yake yenyewe? (Makofi)

Swali la pili, je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye Kata zenye mazingira ya vijijini ambazo ni Rilambo, Shibira, Dilimalitembo, Mletele, Shule ya Tanga, Mwengemshindo, Mbati na Wenje? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwenye swali la kwanza la kuhusu bei ya shilingi 27,000 kwenye sera, naomba kuliarifu Bunge lako kwamba bei zinazotumika kuunganisha umeme kwa wateja wa TANESCO zinapangwa na kusimamiwa na Mamalaka ya Udhibiti ya EWURA. Kwa hiyo, kinachofanywa ni kuangalia maeneo maalum na kuyapangia bei yake. Maeneo ya vijijini ni shilingi 27,000 maeneo ya mijini ni shilingi 321,000 na kuendelea.

Mheshimiwa Spika, ilijaribiwa kufanyiwa shilingi 27,000 kila sehemu lakini kwa uhalisia ilionekana ni ngumu, lakini zoezi la kuendelea kubaini ni kiasi gani kitumike kuunganisha eneo gani kinaendelea kama ambavyo tumekuwa tukitoa taarifa na jambo hilo litakapokamilika basi bei nzuri za kila eneo zitatangazwa ili ziweze kutumika.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili. Kuhusu umeme kupelekwa katika maeneo ya vijijini lakini yaliyoko mijini tunafanya hivyo, kwenye baadhi ya maeneo tayari kuna awamu ya kwanza ilishafanyika kwa Mikoa kadhaa, awamu ya pili imefanyika na sasa inaendelea awamu ya tatu. Nimhakikishie Mheshimiwa Msongozi kwamba katika maeneo aliyoyataja nayo yamo katika plan za Serikali na upatikanaji wa fedha utakavyokuwa tayari maeneo hayo pia yatapelekewa umeme katika maeneo ya mijini yenye uso wa vijijini kwa kadri ya upatikanaji wa fedha katika siku chache zijazo. Nashukuru.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mtwara – Pachani – Luchili – Mkungu – Mtwara Matata – Ligera – Ligunga – Lusewa – Magazine – Lingusenguse – Nalasi – Mbesa mpaka Tunduru ina urefu wa kilometa 305, barabara hii ni ya kimkakati. Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunatambua barabara hii ni kweli ni ya kimkakati na ya kiuchumi, tunachofanya sasa hivi, tulishakamilisha usanifu. Tulichoamua sasa hivi kutokana na urefu wa barabara na umuhimu wa hii barabara, tumeainisha maeneo yote ambayo yanasumbua pamoja na madaraja, tuyaimarishe na kujenga zege ama lami nyepesi ili barabara ile ipitike muda wote wakati huu tunatafuta fedha kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza swali moja dogo la nyongeza lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini Serikali itafanya mapitio upya ya Sheria Na. 263 ya Mwaka 2015 ili kuongeza fidia na pensheni kwa watumishi hao?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tatizo hili ni kubwa ambalo linapelekea kwamba Madaktari na Manesi pindi inapotokea magonjwa ya mlipuko wanakosa ari na moyo wa kufanya kazi kutokana na fidia ndogo ambayo wanaipata. Je, Serikali imefanya utafiti wa kina juu ya tatizo kubwa namna hii? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake amabalo kwa kweli linalenga kuboresha huduma lakini kuwatia ari watumishi wa afya. Kwanza, ameuliza kwamba ni lini Serikali itakaa na kujadili ni namna gani tunaweza kuboresha hili. Hili suala linahitaji siyo Wizara ya Afya peke yake linahitaji Wizara mbalimbali za sekta husika kulingana na tatizo lilivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niwaombe Wabunge kwa sababu mmelisema hili hapa, basi tutaenda kufanya mawasiliano na kukaa na wenzetu na Serikali ikitokea mjadala ndani ya Serikali ikionekana kuna uhitaji huo basi italetwa hapa Bungeni kwa ajili ya kubadilisha, lakini turuhusu kwanza likatazamwe na wataalam ili tuone linaweza kufanywajwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili kwamba watumishi wengi wanaogopa kufanya kazi kwenye maeneo yao, kwa sababu wanaogopa kupata matatizo. Mimi nikwambie tu kwanza nitumie fursa hii kuwapongeza watumishi wa afya Tanzania, tulipata tatizo Kagera watumishi wetu hawakutazama kuna hatari gani wakati watu wengine wanakimbia kwenye majanga wao walikimbilia kwenye eneo la tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania Waziri wetu wa Afya alikwenda Marekani juzi kwenye Umoja wa Mataifa walimpongeza kwa kushangaa ni kwa namna gani ndani ya siku 78 Tanzania imeweza ku-control Marburg. Maana yake hizi ni juhudi za watumishi wetu hawa ambao wana moyo, wana nia njema ya kuwahudumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mnajua wakati wa corona kila mtu alikuwa anakimbia, kila mtu anaogopa kwenda hospitalini lakini watumishi wetu walikimbia na wakafanya na umeona kilichotokea Tanzania na vifo vingi havikuwepo Tanzania kama maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hawa watumishi kwa kweli pamoja na mazingira mengine na matatizo mengine, wanafanya kazi nzuri sana na wana moyo mzuri. Kwa hiyo, nikuambie tu hawaogopi lakini kwa ukweli halisi hebu tukayaangalie haya mengine ambayo umeyasema hapa yaonekane kama kuna sababu ya kufanya hivyo tuende nayo na kuboresha zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wetu amekuwa akimuelekeza Waziri wetu. Kwa mfano, kuna kijana aliyepata shida kule Kagera na Mheshimiwa Rais wetu alielekeza na yule kijana alipewa zaidi ya Shilingi Milioni Kumi, kama incentive tu kupitia masemo wa Mheshimiwa Rais wetu na sasa hivi amaepewa shilingi 10,000,000 yake na anaendelea na shughuli zingine za Kisheria na haki zake za Kisheria bado anaendelea kuzipata. Kwa hiyo, tutaendelea kuwatia moyo kwa namna hiyo, lakini nikuambie tu kwamba Watumishi wana ari sana. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama kwanza kumshuruku Mheshimiwa Naibu Waziri kwa maelezo mazuri, pia nimesimama kumshukuru Mheshimiwa Jacqueline Msongozi kwa swali lake. Nimesimama kwa sababu kipaumbele cha kwanza cha Serikali ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kupambana na magonjwa hatarishi na magonjwa ya mlipuko ni kuwalinda watumishi wa afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatufanyi kitu chochote. Kwanza tunatoa training kwa watumishi wa afya jinsi gani ya kuhudumia wagonjwa wa magonjwa ya mlipuko. Pili, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia anatuwezesha kutoa vifaa kinga vya kutosha kwa ajili ya watumishi wa afya, lakini pale kutakapotokea changamoto amesema vizuri Naibu Waziri Serikali inafanya kila linalowezekana kuokoa maisha ya mtumishi wa afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Kagera tulikuwa na mtumishi Daktari mmoja alipata maambukizi ya Marburg kwa sababu ya kumhudumia mgonjwa, tulipeleka dialysis mashine Kagera, tumepeleka Madaktari Bingwa Saba na Wauguzi Bingwa na leo Daktari yule tumeweza kuokoa maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimesimama kwanza kuwashukuru watumishi wa afya. Watumishi wetu wa afya siyo waoga, hawajawahi kukimbia wagonjwa. Pili, nimesimama kuwahakikishia Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia itatoa kipaumbele cha kuwalinda watumishi wa afya katika kupambana na magonjwa ya mlipuko na magonjwa hatarishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama ili kuweza kuwatia moyo watumishi wa afya, hatujawahi kuona Watumishi wa Afya wamekimbia wagonjwa Tanzania.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bajeti ya Serikali ya 2023/2024 imepanga kutoza asilimia 10 ya mapato ya mnufaika ambaye ni mkulima; kwa nini Serikali isisamehe tozo hiyo kwa wakulima wadogo ili kuwavutia wakulima hao kwenye kuwekeza zaidi kwenye uvunaji wa carbon?

Swali la pili, Mwongozo wa Carbon wa mwaka 2022 umejikita zaidi katika biashara za carbon za misitu mikubwa, lakini Serikali haimtambui mkulima huyu mdogo; je, Serikali itaboresha lini mwongozo huo ili biashara ya carbon kwa wakulima itambulike rasmi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuanzia na swali la kwanza; suala la uwepo wa tozo ni suala ambalo lipo kisheria, lakini jambo la kusamehewa tozo ama kupunguza hiyo tozo pia lipo kisheria. Mimi nimwombe tu Mheshimiwa kwamba atupe muda twende tukakae na Wizara inayohusika, wakiwemo wenzetu Wizara ya Fedha, tuone namna ya kuweza kuzungumza nao ili lengo na madhumuni kuweza kuwapa nafasi wakulima wadogo wakaweza ku-invest zaidi kwenye carbon baada ya kupunguziwa tozo hiyo, kwa sababu biashara hii inalenga zaidi kule kwenye community.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, juhudi ya kwanza ambayo tumeifanya ni kutengeneza kanuni na miongozo, jambo ambalo limeshakamilika. Lakini ni kweli tumeona na tumegundua kwamba kuna baadhi ya mapungufu, na sasa hivi ninavyozungumza tumeshaanza kuzifanyia review kanuni hizi. Hivi ninavyozungumza kuna timu yetu ipo Morogoro imekaa kwa ajili ya kufanya baadhi ya mapendekezo kuongeza vitu ili mradi tuweze kuwapa nafasi wakulima na wengine.

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge baada ya review hii tutaona maboresho makubwa yatakayokuja kugusa kwenye sekta za wakulima, sekta za wafugaji na sekta za wafanyabiashara. Nakushukuru.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wananchi wanaoishi katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Tunduru na Namtumbo wamekumbwa na taharuki kubwa sana wakati wote wa maisha yao kuhusiana na hali halisi ya wingi wa tembo na uharibifu mkubwa unaofanyika, tembo wamefikia hatua ya kufika mpaka majumbani.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwavuna hawa tembo ili waweze kupungua na adha inayowakuta wananchi hawa ipungue? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Msongozi Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la fidia Mheshimiwa Mbunge nimtoe wasiwasi na Wabunge wengine wote. Jana tulikuwa na semina tuliweza kuliongelea hili suala, tulichofanya sisi kama Serikali tumekubaliana na mawazo ya Waheshimiwa Wabunge kwamba tunayachukua kwa umoja wao, tunaenda kuangalia sheria ambayo ilipitisha mwanzo kiwango hicho tuifanyie review kisha tutaleta humu humu Bungeni tuone namna iliyobora ya kuangalia thamani ya hawa wananchi ambao wanapata hasara ya kupoteza mazao na wengine wanapoteza hadi maisha ili angalau hii fidia au kifuta machozi na jasho kiweze kukidhi haja ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, suala lingine la kuhusu taharuki ya tembo, ni kweli hii ni changamoto kubwa na tunawapa pole sana wananchi ambao wamekuwa wakikumbana na changamoto hii ya wanyama wakali hususan tembo. Serikali ina mkakati mahsusi wa kuhakikisha kwamba tunaanzisha vituo viwe karibu sana na maeneo yaliyohifadhiwa ili angalau taharuki hii inapojitokeza basi Askari wawe karibu kutatua tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo tumeendelea kutoa elimu kwa wananchi ili tuwe na ushirikishwaji wa karibu na jamii ili kudhibiti hawa wanyama wakali na waharibifu. Ahsante. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Ni lini Serikali itaongeza wafanyakazi kwa maana ya Matabibu katika Kituo cha Afya cha Matemanga, Nakapanya na Mtakanini?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, maeneo aliyotaja Mheshimiwa Mbunge ni mojawapo ya maeneo ambayo hata sisi tunajua yana watumishi wachache na ni maeneo ambayo wengi wakipangiwa wanahama. Namwomba Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo nilimjibu Mheshimiwa Mbunge mwenzake, kwenye nafasi ambazo ametangaza Waziri wa TAMISEMI ametaja, tukutane tuangalie na sisi upande wa Afya tuweze kuona namna ya kutoa kipaumbele kwa maeneo hayo kwenye hizi nafasi ambazo zilipungua.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, naomba niulize swali moja dogo lenye sehemu (a), (b), (c), (d) kama ifuatavyo: -

SPIKA: Mheshimiwa ni (a) na (b) pekee. Kwa hiyo, katika hayo manne chagua mawili.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante.

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongea na wadau ili waweze kuondoa gharama kubwa iliyopo ya ununuzi wa mtungi wa gesi na gesi yenyewe, wakati mchakato wa kupunguza au kuweka ruzuku kwenye nishati ya gesi unaendelea kwa Serikali?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Shule ya Ufundi Mtwara Tech. imefunga mfumo wa gesi asilia suala ambalo limepunguza gharama kubwa ambayo ilikuwa inatumika wakati wakitumia nishati mbadala ya kuni na mkaa. Wakati wakitumia nishati hiyo walikuwa wanatumia shilingi milioni saba. Sasa baada ya kuweka mfumo wanatumia shilingi milioni 1.8.

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka mfumo huo kwenye Taasisi zote za Serikali ikiwemo Chuo cha Ualimu Matogolo na Shule za Sekondari zote katika Mkoa wa Ruvuma na nchi yote ya Tanzania? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyofuatilia matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la ruzuku, ajenda ya nishati safi ya kupikia ni ajenda ya Mheshimiwa Rais mwenyewe. Wote mnakumbuka wakati wa mkutano wa COP28 Dubai, alizindua Mkakati wa Nishati ya Kupikia kwa Wanawake Afrika. Kwa hiyo, jambo hili tumelibeba kwa uzito sana.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ruzuku tayari tuna programu na miradi kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya tunayo programu ambapo mawakala wanawezeshwa kifedha ili kupunguza bei ya mitungi kwa wale wanunuaji wanaonunua gesi kwa mara ya kwanza. Tutaendelea kubuni miradi na kutafuta fedha ili kuhakikisha wananchi wanapata mitungi ya gesi kwa gharama rahisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, la pili, kuhusiana na kuwekeza mifumo ya gesi katika taasisi; kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) tumeshaanza mradi kwa ajili ya kuweka nishati hii safi ya kupikia ya gesi kwenye magereza, kambi za Jeshi pamoja na shule za msingi na sekondari. Tutaendelea kutafuta fedha ili kuhakikisha tumefikia taasisi nyingi zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa taasisi alizosema za Mkoa wa Ruvuma tutazingatia pia, ili kuhakikisha wanawekewa mifumo hii, ahsante.